Search This Blog

Friday 7 April 2023

SCANDLE (KASHFA) - 1

 






IMEANDIKWA NA : PATRICK CK

***************************************************************

Simulizi : Scandle (Kashfa)

Sehemu Ya Kwanza (1)

 SCANDAL


(KASHFA)


SEASON 1


ARUSHA – TANZANIA


Mahakama kuu kanda ya Arusha ilifurika watu waliofika kusikiliza hukumu ya kesi ya mauaji inayomkabili mkurugenzi wa Mulumbi group of companies Papi Gosu Gosu.Katika kesi hiyo mtuhumiwa Papi Gosu Gosu alidaiwa kumuua kwa kumpiga risasi mwanamitindo na mwandishi wa habari Lidya Kipara kwa kutumia bastola


yake wakiwa katika hoteli ya Kobe Village jijini Arusha.


Jaji Ambola Mkasu akisoma hukumu kwa muda wa saa tatu huku mahakama ikiwa katika utulivu mkubwa,alisema kwamba mahakama iliridhishwa na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka kwamba mtuhumiwa alifanya mauaji hayo kwa kukusudia.Mashahidi sita wa upande wa mashtaka walitoa ushahidi mzito kuthibitisha kuwa mtuhumiwa alitenda kosa hilo.Mawakili nane


wabobezi wa sheria waliokuwa wakimtetea Papi Gosu Gosu walishindwa kuithibitishia mahakama kwamba mteja wao hakutenda kosa la mauaji hivyo mahaka kumtia hatiani


Katika kuhitimisha hukumu hiyo,Jaji Ambola alisema baada ya kupitia kwa umakini ushahidi wa pande zote mbili,mahakama imejiridhisha bila shaka yoyote kwamba mtuhumiwa alitenda kosa hilo la mauaji hivyo anamuhukumu kutumikia kifungo cha maisha gerezani.


Baada ya hukumu kutolewa familia ya marehemu Lidya Kipara walitoka nje ya mahakama wakiwa na nyuso za furaha wakiishukuru mahakama kutenda haki kwa mtuhumiwa aliyemuua binti yao.Kisa Mwakasipa mama mzazi wa Lidya alizungukwa na waandishi wa habari wakitaka kupata maoni yake kufuatia hukumu ile


“Ninaishukuru sana Mahakama imetenda haki kwa muuaji wa mwanangu” akasema Bi Mwakasipa


“Mama unaridhika na adhabu aliyopewa mtuhumiwa? Wengi walitegemea labda ingetolewa adhabu ya kifo” mmoja wa waandishi wa habari akauliza


“Siwezi kuipangia mahakama adhabu ya kutoa.Ninachoshukuru ni kwamba amepewa adhabu kwani hata kama angehukumiwa kunyongwa isingesaidia kumrejesha mwanagu” akasema Bi Mwakasipa na kuvutwa mkono na ndugu zake wakawaacha wale waandishi wa habari.


Baada ya hukumu kutolewa Papi Gosu Gosu alikuwa kimya hakuzungumza lolote akisubiri kupelekwa gerezani.Baadhi ya marafiki na wafanyakazi wa makampuni anayoyaongoza walikuwepo mahakamani na wengi walimwaga machozi baada ya hukumu kutolewa.Mawakili waliokuwa wanamtetea Gosu Gosu walitoka ndani ya mahakama na kuzungukwa na waandishi wa habari wakitaka kupata maoni yao kufuatia hukumu ile.Kiongozi wa jopo lile la mawakili Edmund


msomi akakubali kujibu maswali machache t0ka kwa waandishi wa habari.


“Nataka kufahamu namna mlivyoipokea hukumu hii na kama mmeridhishwa na maamuzi ya mahakama” akauliza mmoja wa waandishi wa habari


“Tumeyapokea maamuzi ya mahakama,sisi kama mawakili wa utetezi tutakaa na kuichambua hukumu hiyo na tutaangalia nini tufanye kuhakikisha kwamba mteja wetu anapata haki yake”


“Mnakusudia kukata rufaa? Akauliza mwandishi mwingine


“Bado hatuna jibu kwa sasa lakini pale tutakapokuwa tumekaa na kujadiliana pamoja na mteja wetu mtafahamu hatua tutakazozichukua” Wakili Edmund Msomi akajibu na kuondoka


Papi Gosu Gosu alitolewa mahakamani na kuingizwa katika gari la magereza ambalo liliondoka na kuelekea katika gereza la Kimondo lililoko eneo la Ngara Mtoni jijini


Arusha.Hili ni gereza lenye ulinzi mkali ambalo ni maalum kwa ajili ya watu waliofungwa kwa makosa ya ujambazi,madawa ya kulevya,mauaji na wale wanaotumikia vifungo virefu gerezani.


MWAKA MMOJA ULIOPITA


Asubuhi siku ya jumatatu,Papi Gosu Gosu aliegesha gari katika maegesho ya ofisi zao jijini Dar es salaam.Wakati akishuka garini aliwaona walinzi wakimvuta


mwanamke mmoja wakimtoa nje ya geti.Katika purukushani zile mkoba wa mwanamke yule ukaanguka na vifaa vilivyokuwamo ndani yake kumwagika chini.Gosu Gosu alikiona kitendo kile na kuwafuata wale walinzi.


“Kuna nini hapa? Akauliza kwa ukali na wale walinzi wakamuachia Yule dada ambaye aliitumia nafasi ile kuokoa vifaa vyake vilivyomwagika chini


“Tumepewa maelekezo na bosi Chuma tumuondoe huyu


msichana nje ya geti”akajibu mmoja wa walinzi


“Amefanya nini? Akauliza “Analeta vurugu eneo la


ofisi bosi” akajibu mmoja wa walinzi


“Hata kama mmepewa maelekezo hampaswi kumtoa mtu ndani kwa mabavu namna hii ! akafoka Gosu Gosu na walinzi wale waliokuwa wamesimama kwa utii wakaitika kwa adabu.Mara akajitokeza Sedekia Chuma mkurugenzi msaidizi wa MGC Ltd


“Mkurugenzi nimelazimika kutumia walinzi kumuiondoa huyu mwanamke ofisini baada ya kugoma kuondoka na kuanza kuleta vurugu”akasema Sedekia


“Si kweli kaka.Yote anayokwambia huyu mtu ni uongo mtupu.Sikuleta vurugu zozote”akasema Yule mwanamke


“Nini kimetokea hapa?


Akauliza Gosu Gosu na mabishano yakaanza ikamlazimu Gosu Gosu kumchukua Yule mwanamke na kwenda naye ofisini kwake.


“Nieleze tafadhali nini kimetokea? Akauliza Gosu Gosu


“Ninaitwa Lidya Kipara ni mwandishi wa habari.Nimefika hapa katika kampni yenu kuomba udhamini katika bonanza la wanahabari litakalofanyika hapa Dar es salaam.Nilielekezwa nikaonane na ndugu Chuma nikamueleza shida yangu akasema kwamba yupo tayari kutusaidia udhamini lakini katika fedha atakazotoa kama udhamini nusu zitakuwa zake


na nusu zitakazobaki ndizo tutumie katika kuandaa bonaza letu.Kama haitoshi alianza pia kunitongoza na kutishia kama nisipomkubali hatuwezi kupata udhamini.Hapo ndipo nilipokasirika na tukaanza kutoleana maneno machafu akawaita walinzi wakaja kunitoa ofisini kwake” akasema Lidya


“Pole sana Lidya” akasema Gosu Gosu na kufungua kabati akatoa kitabu cha hundi


“Kiasi gani mnahitaji?


Akauliza


“Tunahitaji kiasi chochote ambacho mnaweza mkatudhamini” akajibu Lidya


Gosu Gosu akaandika hundi na kumpatia


“Milioni kumi naamini zitawasaidia” akasema GosuGosu


“Nakushukuru sana kaka kwa msaada huu mkubwa” akasema Lidya


“Pole kwa masahibu yaliyokukuta.Siku nyingine mnapohitaji msaada wa udhamini naomba unione mimi mwenyewe” akasema


Gosu Gosu na kuchukua kadi yake ya biashara akampatia Lidya


“Chukua kadi hii muda wowote ukihitaji kuwasiliana nami kwa msaada wowote usisite kunipigia” akasema Gosu Gosu na kuagana na Lidya akaondoka


****************** “Bravo do you miss


Mathew? Gosu Gosu


akamuuliza Bravo mbwa wa Mathew Mulumbi mwenye mafunzo makubwa.Ni saa tatu


za usiku tayari Gosu Gosu amekwisha rejea nyumbani akitokea kazini na kama ilivyo kawaida yake kila jioni hupenda kukaa na Bravo nje ya nyumba akijipumzisha.


“Kama ungeweza kuongea najua ungesema but I know you do miss him.Me too I miss him so much” akasema Gosu Gosu akionekana kama vile anazungumza mwenyewe kwani Bravo hakuweza kujibu chochote alikuwa amejielekeza katika bakuli lililokuwa na chakula


“Sifahamu alipo Mathew hadi sasa.Imekwisha pita miaka mitatu hatujawahi kuwasiliana na hakuna anayefahamu mahala alipo.Ninachoamini ni kwamba siku moja atarejea nyumbani.Hata kama itapita miaka mingi lakini lazima siku moja atarejea nyumbani” akasema Gosu Gosu na kunywa funda la kinywaji


“Sina hakika kama anafahamu mpenzi wake Ruby ameolewa na Rais mstaafu Fabian Kelelo.Lakini ni yeye mwenyewe aliyempa Ruby


ruhusa ya kuendelea na maisha yake.Yawezekana atakaporejea kutoka huko aliko atakuwa tayari na mke” Gosu Gosu akatolewa mawazoni baada ya simu yake iliyokuwa pembeni kuita.Zilikuwa ni namba ngeni katika simu yake


“Hallow” akasema Gosu Gosu


“Kaka habari za usiku huu.Mimi ni Yule dada uliyeniandikia hundi ya fedha asubuhi”


“Ouh Lidya” akasema Gosu Gosu huku akitabasamu


“Kumbe bado unalikumbuka jina langu”


“Siwezi kulisahau.Bado ninakukumbuka”


“Nashukuru kaka.Nimekuipigia kukushukuru tena kwa msaada ule mkubwa na wenzangu wamenituma nikushukuru na nikuombe kama utapata nafasi siku ya bonanza uhudhurie ili tukushukuru wewe pamoja na wafadhili wengine mliosaidia katika kufanikisha bonanza letu” akasema Lidya


“Hakuna tatizo nitahudhuria.Utanijulisha siku na mahali”


“Ahsante sana kaka kwa wema wako.Yaani mpaka sasa bado sijaamini”


“Nami nakushukuru pia kwa kitendo chako cha kukataa maombi ya Yule jamaa aliyetaka kujipatia fedha kupitia jambo hili.Endelea na moyo huo wa kukataa mambo machafu kama yale” akasema Gosu Gosu


“Haya ahsante kaka usiku mwema” akasema Lidya na kuagana na Gosu Gosu.


“Sikujua kumbe kuna wizi mkubwa unafanyika kupitia mambo haya ya udhamini au ufadhili wa jambo Fulani.Inaandikwa fedha nyingi imefadhili jambo Fulani kumbe ni robo au nusu yake ndiyo inakwenda sehemu husika iliyobaki inaingia mifukoni mwa watu.Kama Sedekia asingekiri na kuomba msamaha ilikuwa nimtimue kazi leo hii hii lakini aliomba sana msamaha na kukiri kosa lake” akawaza Gosu Gosu


SIKU 5 BAADAE


Bonanza kubwa lililowahusisha wana habari wa mkoa wa Dar es salaam lilifanyika siku ya jumamosi na kufana sana.Kulikuwa na michezo mingi na mashindano mbali mbali yakihusisha timu za mashirika mbali mbali ya habari.Saa kumi na moja za jioni mgeni rasmi ambaye ni naibu waziri wa habari akatoa zawadi kwa washindi mbali mbali walioshinda katika mashindano tofauti tofauti na baada ya zoezi hilo kukamilika


wanahabari wakapata fursa ya kujimwaga ukumbini kucheza muziki.


Gosu Gosu alifika katika bonanza hilo wakati mgeni rasmi akigawa zawadi na baada ya mgeni rasmi kuondoka akamtumia ujumbe Lidya akamjulisha kwamba tayari amekwisha fika.Lidya akamfuata mahala alipo wakasalimiana.Akiwa mmoja wa waandaaji wa bonza lile Lida alijawa na furaha kwa mambo yote kwenda vizuri kiasi cha kusifiwa na kila mshiriki.


“Nilidhani hutafika” akasema Lidya wakiwa wamekaa sehemu


“Nilichelewa,nilikuwa na kikao muhimu cha kazi hata hivyo nimelazimika kuahirisha kikao hicho hadi siku ya jumatatu baada ya kuona muda unakwenda na ninazidi kuchelewa.Mimi huwa ni mtu wa kuimiza ahadi.Utanisamehe kwa kuchelewa” akasema Gosu Gosu na mara Lidya akafuatwa akaitwa


“Siku ile nilipomuona Lidya yawezekana macho


yangu hayakuwa yakiona sawa sawa.Mbona naona leo hii uzuri wake umetia fora?


Namuona kama Lidya wa leo na Yule wa siku ile ni tofauti kabisa.Mtoto mzuri sana huyu” akawaza Gosu Gosu na baada ya muda Lidya akarejea


“Samahani sana kaka kwa kukuacha mwenyewe”


“Papii.Niite Papi au ukipenda Gosu Gosu inatosha” akasema Gosu Gosu


“Sawa Gosu Gosu.Unajua mimi ni mmoja wa waandaaji hivyo ninaitwa mara kwa mara”


“Usijali ninaelewa.Hata hivyo hongera sana Lidya kwa bonanza hili lililofana sana”


“Mliofanikisha bonanza hili likafana ni ninyi ambao mmeharibu mipango yenu na kutupa sisi fedha za kujumuika hapa.Ahsante sana kwani wewe ni mmoja wao” akasema Lidya


“Nashukuru Lidya” akasema Gosu Gosu na kunyamaza baada ya watu wawili kumfuata Lidya wakamjulisha kuwa anatakiwa.Lidya akamuomba samahani Gosu Gosu


akaondoka na baada ya muda akarejea


“Ninaona aibu Gosu Gosu kwa kukuacha peke yako.Natamani tuhame hapa tukakae mahala ambako hakuna usumbufu” akasema Lidya


“Usijali Lidya ninaelewa wewe ni mmoja wa waandaaji hivyo usumbufu kama huu lazima utatokea.Labda kama hutajali baada ya kumaliza shughuli zako tunaweza kukutana mahala kwa ajili ya kupata chakula na maongezi kidogo ili niweze kukuacha


uendelee na majukumu” akasema Gosu Gosu


Ushauri ule wa Gosu Gosu Lidya akaukubali kwa miadi ya kukutana saa mbili usiku kwa kwa chakula na maongezi.Gosu Gosu akaondoka akiwaacha wanahabari wakisakata rhumba


************* “Nahisi kama kuna


sumaku inanivuta kuelekea


kwa Lidya.Toka nimeonana naye jioni ya leo kule ufukweni


sijielewi elewi.Nimejikuta kila wakati ninatamani niwe naye” akawaza Gosu Gosu akimalizia kujiandaa kwa ajili ya kwenda kukutana na Lidya kama walivyokuwa wamekubaliana.Alijitazama akaridhika kwamba amependeza vya kutosha halafu akaelekea katika gari lake na kuondoka.


“Nimekuwa mwoga sana wa kuingia katika mahusiano yoyote kwani kila wakati nimekuwa nikiishia kuumizwa lakini ninahisi kama Lidya anakuja kwa kasi kubwa


kichwani kwangu.Ngoja niendele naye taratibu nione nitafika naye wapi japo kwa muda huu mfupi niliokaa naye nimegundua mambo mengi kwake.Ana upekee mkubwa” akawaza Gosu Gosu akiwa garini


Gosu Gosu alifika mahala alipokubaloiana akutane na Lidya akamchukua wakaondoka


“Lidya najua umechoka kwa maandalizi hivyo tunakwenda kupata chakula na kisha nitakurudisha nyumbani”


“Usihofu Gosu Gosu hakuna uchovu mambo haya ni ya kawaida tumekwisha yazoea”


“Bonanza hili huwa mnalifanya kila mwaka?


Akauliza Gosu Gosu “Ndiyo limekuwa


likifanyika kila mwaka lakini ni mara yangu ya kwanza nimeingia katika kamati ya maandalizi”


“Hongereni mmejitahidi sana.Japo nilifika kwa kuchelewa lakini bonanza lilifana sana”


“Ahsante” akajibu Gosu Gosu na simu ya Lidya ikaita akaipokea


Lidya alizungumza na mtu simuni hadi walipofika katika hoteli ambako Gosu Gosu alipanga wale chakula usiku ule.Baada ya kuegesha gari ikamlazimu Lidya kumuaga mtu aliyekuwa anazungumza naye simuni akaongozana na Gosu Gosu kuelekea sehemu ya chakula.


Walihudumiwa haraka na wahudumu wachangamfu.Mara tu


walipoanza kula simu ya Lidya ikaita akaizima


“Samahani nilisahau kuzima simu”akasema Lidya


“Usijali Lidya.Watu kama ninyi simu zenu zinapaswa kupatikana muda wote” akasema Gosu Gosu


“Nakubali lakini kuna nyakati za kupumzika vile vile” akasema Lidya


“Unafanya kazi kampuni gani ya habari?


“Ninafanya kazi gazeti la Fukufuku.Ninaandika habari za kiuchunguzi” akajibu Lidya


“Ouh hongera sana.Kuna wanahabari wachache sana siku hizi wanaoandika habari za kiuchunguzi .Wengi wana hofu ya usalama wao”akasema Gosu Gosu


“Ni kweli.Unapofanya habari za uchunguzi wa kina unayaweka maisha yako hatarini.Wapo wanahabari wengi tu wamekwisha poteza maisha kutokana na mambo haya ya kulifuatilia jambo kwa kina hasa yale yanayowahusu watu wazito” akasema Lidya


“Wewe huogopi? Uandishi wa uchunguzi ni kama


upelelezi”Akauliza Gosu Gosu na Lidya akacheka kidogo kisha akajibu


“Mimi ninamtanguliza Mungu katika kazi yangu ndiye anayeniwezesha nikaifanya vizuri” akajibu Lidya


“Kwa nini usiachane na hiyo kazi nikakupa kazi katika kampuni yangu? Akauliza Gosu Gosu


“Ninashukuru kwa hilo lakini kazi hii ninaipenda sana.Hata wazazi wangu wamejaribu sana kunishawishi nibadili fani ila ninapenda uandishi wa habari”


“Vizuri sana inapendeza kama ukifanya kazi ambayo unaipenda”akasema Gosu Gosu


Gosu Gosu na Lidya waliendelea na mazungumzo yao hadi ilipofika saa tano za usiku ndipo Gosu Gosu alipomrejesha Lidya nyumbani kwake.


“Watoto wa mjini wanaweza wakasema ninatumia kizizi kwani nina bahati ya kukutana na kuwa na ukaribu na mabinti wazuri.Hata hivyo kwa wale wote niliowahi kuwa nao


katika mahusiano kwa huyu Lidya nimefunga breki.Ni mwanamke mwenye sifa za kipekee.Ni mwanamke ambaye kila mwanaume angependa kuwa naye.Ni mcheshi,mchapakazi,mbunifu, licha ya uzuri wake wa asili lakini amejaa adabu.Kinywa chake kina sifa ya kuchagua maneno ya kusema.Lazima nianze harakati za kumpata huyu mrembo.Nitakwenda hadi mwisho wa dunia hadi nihakikishe amekuwa wangu” akawaza Gosu Gosu akiwa njiani kurejea nyumbani


kwake baada ya kumrejesha Lidya


BAADA YA MIEZI 9


Ilimchukua Gosu Gosu miezi tisa kupata jibu kutoka kwa Lidya kukubali ombi lake la kuwa wapenzi.Penzi zito lilichipua na kuanza kumea kwa kasi kubwa kama mmea uotao katika ardhi yenye rutuba ya kutosha.Penzi la Gosu Gosu na Lidya lilikuwa ni moja ya penzi lenye afya ya kutosha ambalo mbegu yake ilipandwa katika mioyo yenye


rutuba.Kila mmoja alimpenda mwenzake kupindukia.


Japo Gosu Gosu alikuwa tayari kufunga ndoa mapema lakini ni Lidya aliyemuomba wajipe muda wa kutosha kila mmoja kumfahamu vyema mwenzake kabla ya kuingia katika ndoa.Hili halikuwa tatizo kwa Gosu Gosu alikubali kuvumilia hadi pale Lidya atakapokuwa tayari.


Miezi mitatu toka kuchipua kwa penzi lao,Gosu Gosu alimuomba Lidya waambatane kwenda Arusha katika sherehe za ufunguzi wa


tawi la kampuni ya MGC Ltd. Ilikua ni safari yao ya kwanza wakiwa wapenzi nje ya mkoa wa Dar es salaam.Waliondoka na ndege ya shirika la ndege la Tanzania hadi Arusha wakafikia katika moja ya hoteli kubwa jijini Arusha ijulikanayo kama Kobe Village.


Ulikuwa ni usiku wa kwanza wa Gosu Gosu na Lidya pamoja na kwa mara ya kwanza toka wakiwa wapenzi Lidya alikubali wakutane kimwili.


************


“Ahsante sana Lidya” akasema Gosu Gosu akizichezea nywele za Lydia wakiwa kitandani


“Unashukuru kwa kipi Gosu Gosu? Akauliza Lidya


“Kwa kuja katika maisha yangu.Huwezi jua ni kwa namna gani umenifanya niwe na furaha katika maisha yangu.Ahsante pia kwa usiku wa jana ambao naweza kuuita ni usiku wa dhahabu” akasema Gosu Gosu.LIdya akambusu Gosu Gosu na kusema


“Gosu Gosu ninakupenda sana.Ni Mungu pekee mwenye uwezo wa kusoma mioyo yetu ndiye anayejua ni kiasi gani ninakupenda.Nimewakataa wengi lakini kwako ulimi wangu umekosa nguvu ya kutamka neno hapana.Gosu Gosu naamini utaulinda moyo wangu..”


“Usihofu kuhusu hilo.Ninakuhakikishia Lidya kwamba moyo wako uko sehemu salama.Nitakulinda kama Nyuki wanavyomlinda malkia wao” akasema Gosu Gosu


“Una maneno matamu kama nini” akasema Lidya na wote wakacheka.


“Lidya sitaki uamke leo.Nataka uendelee kulala nitakwenda kukuandalia kifungua kinywa mimi mwenyewe.Wewe ni malkia wangu na lazima nikuhudumie kwa kila kitu”


“C’mon Gosu Gosu.Huoni tutachelewa ofisini”


“Ufunguzi ni baadae mchana wa leo hivyo usihofu tutawahi” akasema GosuGosu akainuka na kuelekea jikoni kwani walikuwa wamekodisha


nyumba nzima hawakutaka usumbufu.Katika hoteli hii kubwa ya Kobe kulikuwa na huduma ya kupangisha nyumba nzima kwa wale wageni ambao wanapenda waishi maisha ya kawaida kama nyumbani


Gosu Gosu akaingia jikoni na kuanza kuandaa kifungua kinywa.Kabla hawajafika alikwisha toa maelekezo ya vitu ambavyo angependa viwepo katika nyumba hivyo hivyo kila alichokihitaji kwa ajili ya asubuhi ile kilikuwepo


“Mapenzi yana raha pale umpate anayekupenda.Ninajiona kama niko peponi kwa namna mimi na Lidya tunavyopendana.Najiona mwenye bahati sana.Ahsante Mathew Mulumbi kwani ni wewe uliyenifikisha hapa na sasa ninaweza kukutana na malaika kama hawa” akawaza Gosu Gosu huku akikoroga mayai


Alimaliza kuandaa kifungua kinywa akapanga vizuri katika sinia halafu akatoka kuelekea chumbani.


“Unapokuwa na mwanamke mzuri anayekupenda inapendeza ukimdekeza.Nitamfanya Lidya kama malkia.Sioni aibu hata kumbeba hadharani ikibidi”akawaza Gosu Gosu huku akitabasamu.Akakinyonga kitasa cha mlango


“Breakfast on be……………..” akasema Gosu Gosu baada ya kuufungua mlango mara sinia alilokuwa amelibeba mkononi likamponyoka na kuanguka.Lidya alikuwa


amelala kitandani akiwa mtupu huku mashuka yote meupe yakiwa yamechafuka damu.


“Lidya !! akapiga kelele Gosu Gosu na kumfuata Lidya pale kitandani.


“Lidya ! Lidya !! akaita Gosu Gosu huku akimtikisa Lidya lakini hakujibiwa.Tayari Lidya alikwisha kufa.Gosu Gosu akamkumbatia huku akilia


“Lidya ! Lidya ! Lidya !


Please wake up ! akaendelea kulia.Gosu Gosu alishindwa kuinuka pale kitandani


alipokuwa amelala Lidya.Haikuwa rahisi kuamini kama ni kweli Lidya ameuawa.Ni muda mfupi tu alimuacha kitandani akaingia jikoni kumuandalia kifungua kinywa na anaporudi anamkuta ameuawa.


“Hiki ni kiini macho.Hili ni jambo lisilowezekana.Ouh Lidya ! akasema Gosu Gosu na mara akagusa kitu kigumu pale kitandani akafunua shuka na kukuta bastola.Moyo ulitaka kumpasuka pale alipoiona bastola ile ikiwa imefanana na bastola yake


ambayo aliiacha nyumbani kwake Dar es salaam.


“Hii mbona kama bastola yangu? Hiki ni kitu gani? Hii ni ndoto au ni jambo la kweli? Akajiuliza Gosu Gosu na kuishika bastola ile iliyokuwa imefungwa kiwambo cha kuzuia sauti akaitazama machozi yakamdondoka


“Hii bastola ndiyo imetumika kutoa uhai wa Lidya ! akawaza Gosu Gosu huku mikono yake ikimtetemeka.Akamtazama tena Lidya ni kweli alikuwa


amefariki.Alipigwa risasi mbili kifuani .


“Haya mbona ni majabu ya karne.Nani amefanya mauaji haya? Milango yote imefungwa na sijasikia mtu mwingine yoyote akiingia humu ndani.Nini hiki kinachoendelea humu ndani?


Akajiuliza Gosu Gosu.Alichanganyikiwa.


Haraka akaishika ile bastola na kutoka mle chumbani akaikagua milango yote ya ile nyumba ilikuwa imefungwa.Wakati akikagua dirisha akamuona mlinzi


aliyevaa sare za bluu za kampuni binafsi ya ulinzi amekaa kitini akiwa na rungu mkononi.Akaufungua mlango na kumfuata Yule mlinzi ambaye alistuka sana alimuona Gosu Gosu akiwa amechafuka damu na mkononi akiwa na bastola.Rungu likamdondoka.Gosu Gosu aliyekuwa na hasira kama Mbogo majeruhi akamnyooshea bastola mlinzi Yule ambaye alikuwa anatetemeka kwa woga.


“Nataka uniambie nani walio ingia humu ndani muda


mfupi uliopita? Akauliza Gosu Gosu huku midomo yake ikimtetemeka kwa hasira


“Sijaona mtu yeyote aliyeingia humo ndani ! akasema Yule mlinzi


“Nitakuua! Niambie ukweli ! akafoka Gosu Gosu.


“Kweli hakuna mtu yeyote aliyeingia humo ndani.Nimekuwa hapa kuanzia saa kumi na mbili za asubuhi na hakuna mtu yeyote aliyefika hapa ! akasema Yule mlinzi.


“Ouh Mungu wangu kitu gani hiki kimenitokea mimi?


Akasema Gosu Gosu halafu akarejea ndani hadi chumbani.


“Hii si ndoto ni kweli kabisa Lidya ameuawa.Kama hakuna mtu aliyeingia humu ndani nani kafanya mauaji haya? Hii bastola imetoka wapi? Kama hakuna aliyeingia humu ndani je Lidya amejiua mwenyewe? Akajiuliza Gosu Gosu na kupiga magoti pembeni ya kitanda akimtazama Lidya.Alichanganyikiwa hakujua afanye nini.


Akiwa bado katika hali ya kuchanganyikiwa mara


akasikia vishindo vya watu wakiingia mle chumbani.Akainyakua ile bastola na kuielekeza mlangoni akajikuta akitazamana na askari polisi wenye silaha


“Weka silaha yako chini tafadhali ! Gosu Gosu akaamriwa


“Jamani sijaua mimi.Nisaidieni kumpata muuaji ! akasema Gosu Gosu


“Weka chini silaha yako ! akaamuru mmoja wa wale askari aliyekuwa


amemuelekezea Gosu Gosu bunduki


“Oh Mungu wangu !! akasema Gosu Gosu na kuiweka chini ile bastola


“Inua mikono juu ! akaamriwa.


Gosu Gosu akainua mikono juu askari wakamfuata na kumfunga pingu


GEREZA LA KIMONDO


Papi Gosu Gosu alifikishwa katika gereza la Kimondo akasajiliwa kama mfungwa mpya halafu akapewa sare za gereza akavaa na askari magereza wakampeleka katika chumba alichopangiwa.Walipita katika vyumba vya wafungwa ambao muda huo walikuwa vyumbani mwao.Miluzi mingi ikasikika wafungwa wakishangilia.Ni kawadia katika gereza hili kuwa na shangwe kila pale mfungwa mpya


anapoletwa.Askari magereza walimuongoza Gosu Gosu aliyekuwa amevungwa pingu hadi katika chumba alichopangiwa mlango wa chuma ukafunguliwa akaingizwa ndani.Kulikuwa na vitanda viwili mle ndani na katika kitanda cha chini mmoja alikuwa amejilaza akisoma biblia.Mara tu Gosu Gosu alipoingia mtu Yule akainuka


“Mchungaji leo tumekuletea mgeni” akasema mmoja wa askari magereza ambaye alionekana


kufahamiana na Yule mtu aliyekuwamo katika kile chumba alimoingizwa Gosu Gosu


“Huyu ni mwenzako utaishi naye humu chumbani atakusaidia kufahamu taratibu za hapa gerezani” Mmoja wa askari magereza akamwambia Gosu Gosu huku akimfungua pingu.Askari wengine wawili wakiwa na silaha zao walizielekeza kwa Gosu Gosu wakati akifunguliwa pingu kwani tayari alikwisha wekewa alama kwamba ni mtu hatari


“Karibu ndugu yangu.Weka vifaa vyako hapa” akasema Yule mchungaji akimuelekeza Gosu Gosu sehemu ya kuweka baadhi ya vifaa alivyopewa kwa ajili ya matumizi yake pale gerezani lakini Gosu Gosu hakujibu kitu, akaweka vile vifaa halafu akakitazama kile chumba kilivyo kidogo akatikisa kichwa kwa masikitiko akapanda kitandani akajilaza na kuvuta pumzi ndefu.


“Yametimia” akawaza Gosu Gosu


“Si ndoto tena bali imekuwa kweli.Maisha yangu yamebadilika na sasa ninakwenda kuozea gerezani.Ninamwachia Mungu haya yote yeye ndiye anayeufahamu ukweli na atanilipia.Sikufanya kosa la mauaji ambalo limenileta hapa gerezani kwa maisha yangu yote yaliyobakia.Sikumuua Lidya” akawaza na kuhisi uchungu mwingi sana na pembeni ya macho yake kukawa na michirizi ya machozi.


“Mimi ni mwanajeshi ni mtu jasiri sipaswi kutoa machozi lakini kwa hili lililonikuta limeniumiza sana na ninashindwa kuvumilia” akawaza Gosu Gosu na kufuta machozi


“Hata hivyo ninacho hitaji hivi sasa ni kujitahidi kukubaliana na hali hii na kuyazoea maisha yangu mapya.Hakuna namna ninavyoweza kutoka tena humu gerezani.Mawakili wangu wanataka kukata rufaa lakini itakuwa ni kujisumbua bure hakuna wanachoweza


kukifanya tena kunitoa katika shimo hili” akaendelea kuwaza.


“Tangu kesi ilipoanza kusikilizwa nilijua tu siwezi kushinda kwani kulikuwa na kila aina ya ushahidi unaoonyesha nilifanya mauaji yale na kibaya zaidi ni bastola yangu ndiyo iliyofanya mauaji yale.Hakukuwa na namna ambayo ningeweza kukwepa kutiwa hatiani.Lakini nani amenifanyia jambo hili baya?Nini malengo yake?


Akajiuliza


“Mtu aliyenifanyia hivi ni mtu anayenifahamu vyema na si mtu mdogo.Ni mtu mwenye nguvu na mtandao mpana sana.Hata watu waliotekeleza mauaji yale walikuwa wataalamu wa hali ya juu mno kwani hawakuacha alama yoyote mle ndani.Kwa hiki kilichonikuta sasa nimekubali kwamba kuna watu wengi ambao hufungwa magerezani kwa makosa ambayo hawakuyatenda.Mambo haya nimekuwa nikiyasikia kwa watu lakini na mimi leo ninaanza kutumikia adhabu ya


kifungo cha maisha gerezani kwa kosa ambalo sikulitenda.Aliyenifanyia hivi ni wazi anataka kunipoteza kabisa.Nimewaza mno nani anayeweza kunifanyia hivi nimekosa jibu” Bado kichwa cha GosuGosu kilijaa mawazo mengi


“Ngoja nilale kidogo nipumzishe kichwa changu ambacho naona kama kinataka kupasuka kwa mawazo” akawaza Gosu Gosu


***********


Kengele ya kuashiria ni muda wa chakula cha usiku ililia na milango ikafunguliwa ili wafungwa watoke vyumbani mwao kwenda katika bwalo la chakula.


“Ndugu yangu ni muda wa kwenda kupata chakula cha usiku” Mchungaji akamwambia Gosu Gosu


“Sihitaji chakula” akasema Gosu Gosu


“Ndugu yangu hapa chakula ni lazima.Sikushauri ukaacha kula chakula.Hata


kama huna hamu cha chakula twende ukachukue chakula na unipe mimi nile” akasema Yule mchungaji na mara akapita askari magereza na kumkuta Gosu Gosu juu ya kitanda akamtaka aamke na aelekee katika bwalo la chakula.Taratibu Gosu Gosu akainuka akaongozana na mchungaji kwenda kupata chakula.


Gosu Gosu akaelekezwa kupanga mstari huku mchungaji akienda kuchukua kipaza sauti na kuombea chakula kile.Gosu Gosu


alichukua chakula katika sinia na kwenda kukaa katika meza ambayo haikuwa na mtu akakitazama kile chakula na kabla hajaamua ale au aache jamaa mmoja akamfuata na kumtaka atoke katika ile meza kwani ina watu.Gosu Gosu akamtazama hakumjibu kitu Yule jamaa akaondoka.Gosu Gosu akaendelea kutazama kile chakula na mara akashikwa bega na mkono mzito akageuka.


“Inuka katafute meza nyingine ! akasema kwa ukali jamaa mmoja mfupi mwenye


mwili uliojaa.Alikuwa mweusi na sura yake ilitisha.Mara wakatokea tena watu wengine watatu wakiwa na masinia ya chakula wakaizunguka ile meza.


“Wewe kiziwi?


Nimekwambia toka hapa katafute meza nyingine ! akafoka Yule jamaa mweusi.Gosu Gosu hakumjibu kitu.


“Huyu ni mgeni hapa gerezani halafu anaonekana ana kiburi.Anatakiwa afundishwe kuwa na adabu kwa wakubwa zake ! akasema


jamaa mwingine na mara akajitokeza mchungaji


“Samahani wakuu huyu ni mgeni amefika leo na haelewi taratibu za hapa” akasema mchungaji na mmoja wa wale jamaa akamkaba shingo


“Unapaswa kumfundisha taratibu za hapa ! akasema Yule jamaa na kumnasa kofi zito mchungaji akaanguka chini .Kitendo kile kikamkasirisha sana Gosu Gosu akageuka kwa haraka na kuidaka shingo ya Yule jamaa mfupi mweusi akamvuta na kukipiga kichwa chake katika


meza ile ngumu.Kwa haraka akapanda juu ya meza na kumrukia teke zito Yule jamaa aliyempiga kofi mchungaji akaanguka chini.Yule jamaa mfupi huku damu ikimtoka usoni baada ya sehemu ya pengeni ya jicho kuchanika akamfuata Gosu Gosu na kuruka ili amvamie lakini Gosu Gosu alimuona na kumkwepa akaanguka chini kama furushi akamfuata na kumtandika teke zito usoni mdomo ukajaa damu.Watu wote waliacha kula chakula wakaanza kushangilia namna


Gosu Gosu alivyokuwa anatembeza kipigo kwa jamaa wale ambao walijiita wakuu wa gereza.


Kikosi cha askari wa kutuliza ghasia gerezani kikafika na kutawanya vurugu ile.Gosu Gosu na wale jamaa wakachukuliwa na kwenda kufungiwa katika vyumba vingine.Ilikuwa ni faraja kubwa kwa wafungwa kwa kitu alichokifanya Gosu Gosu kwani kikundi kile cha wale watu wanne kimekuwa kikifanya unyanyasaji mkubwa sana ndani ya gereza na hata


askari magereza walionekana kuwaogopa.


Gosu Gosu akahojiwa chanzo cha vurugu zile akaeleza kila kitu kilivyokuwa akapewa adhabu ya kufanya usafi chooni siku inayofuata na akatakiwa kuwa makini pale gerezani kisha akarudishwa katika chumba chao


“Pole sana.Hawajakuumiza wale jamaa? Akauliza mchungaji


“Hapana” akajibu Gosu Gosu na kupanda kitandani


“Siku ya kwanza gerezani imeanza kwa namna hii.Wale


jamaa hawanifahamu kama mimi ni mtu mbaya kuliko wao.Hawajui yaliyonikuta hivyo wakae mbali kabisa na mimi.Kwa sasa siogopi hata kutoa roho ya mtu kwani maisha yangu yamekwisha haribika.Tayari nimekwisha pata picha ya namna ya kuweza kuishi katika gereza hili lakini napaswa kuwa makini mno.Gereza hili limejaa wahalifu wa kila namna” akawaza Gosu Gosu na kustuliwa na mchungaji


“Ndugu ninataka kufanya maombi ya usiku kabla ya


kulala hivyo samahani kama nitakukera” akasema Yule mchungaji na Gosu Gosu akamruhusu aendelee


Baada ya maombi mchungaji akamwambia Gosu Gosu


“Uwe na usiku mzuri ndugu yangu japo hatujafahamiana hata kwa majina”


“Naitwa Gosu Gosu” “Mimi ni mchungaji Peter


Msavu”


“Wewe ni mchungaji kweli wa kanisa au cheo hicho


umepewa humu gerezani?


Gosu Gosu akauliza


“Mimi ni mchungaji kabisa wa kanisa” akajibu mchungaji Peter na Gosu Gosu akainuka kitandani akakaa


“Nadra sana kusikia mtumishi wa Mungu amefungwa gerezani.Ulifanya nini hadi ukafika hapa gerezani? Akauliza Gosu Gosu


“Nilimpa mimba mwanafunzi wa kidato cha pili nikahukumiwa kifungo cha miaka thelathini gyerezani” akajibu mchungaji Peter


“Ni kweli ulitenda kosa hilo au ulitengenezewa kesi?


Akauliza Gosu Gosu


“Hapana sikutengenezewa kesi.Ni kweli nilitenda kosa hilo.Nilikuwa na mahusiano na huyo mwanafunzi wa shule ya sekondari hadi akapata mimba.Mimi kama mchungaji nafahamu kutoa mimba ni kosa mbele za Mungu hivyo sikuwa tayari binti Yule atoe mimba nikakubali kubeba adhabu hii.Nilitenda kosa na ninastahili adhabu” akasema mchungaji Peter akionyesha


masikitiko makubwa kwa kosa alilolifanya


“Ninajutia sana kwa kitu nilichokifanya.Hivi sasa familia yangu inateseka,watoto wangu wanashindwa kusoma kutokana na ujinga wangu mimi.Inaumiza mno ndiyo maana ninafunga siku tatu kwa juma kumuomba Mungu anisamehe kosa hili” akasema mchungaji Peter na ukimya ukapita.


“Gosu Gosu wewe umefanya kosa gani hadi ukaletwa hapa? Akauliza mchungaji Peter


“Nimefungwa maisha kwa kosa la mauaji” akasema Gosu Gosu na ukimya ukatanda mle ndani


“Pole sana” akasema mchungaji Peter


“Sikutenda kosa.Sikuua mtu” akasema Gosu Gosu.


“Hukuweka wakili wa kukutetea? Akauliza mchungaji Peter


“Nilikuwa na mawakili nane nguli wa sheria lakini hawakuweza kuishawishi mahakama kwamba sikutenda kosa nikatiwa hatiani na


kufungwa kifungo cha maisha” akasema Gosu Gosu


“Gosu Gosu wewe ni mkristu? Akauliza mchungaji Peter


“Sifahamu mimi ni dini gani japo nakumbuka mara chache niliwahi kuingia kanisani wakati nikiwa mdogo sana”


“Gosu Gosu mambo haya yaliyokukuta yanawakuta watu wengi zama hizi na yalitabiriwa katika biblia” akasema mchungaji Peter na kufungua biblia yake


“Katika 2Tim.3:1-5 inasema hivi; Lakini ufahamu neno hili,ya kuwa siku za mwisho kutakuwako na nyakati za hatari .Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe,wenye kupenda fedha,wenye kujisifu,wenye kiburi,wenye kutukana,wasiotii wazazi wao,wasio na shukrani,wasio safi,wasiowapenda wa kwao,wasiotaka kufanya suluhu,wasingiziaji,wasiojizuia


,wakali,wasiopenda mema,wasaliti,wakaidi,wenye kujivuna,wapendao anasa


kuliko kumpenda Mungu” Gosu Gosu haya yote yalitabiriwa katika maandiko hivyo nakuomba ndugu yangu usivunjike moyo.Kama kweli hukutenda kosa Mungu anaona na atakusimamia dhidi ya wale wote waliokusababishia ukafika hapa.Mkabidhi Mungu maisha yako na usiache kumuomba.Kama hutajali ninaweza kuanza kukupa msaada wa kuyafahamu maandiko yatakupa faraja kubwa na utagundua kwamba hata kama wanadamu


wamekutenda jambo baya lakini Mungu wa mbinguni anakupenda na atayafanya maisha yako hapa gerezani yawe mepesi.Kama waliokusingizia walitaka uteseke nakuhakikishia Mungu atawaumbua na ninakuhakikishia siku moja utatoka humu gerezani” akasema mchungaji Peter


“Peter nahitaji kupumzika.Tutazungumza kesho” akasema Gosu Gosu na mchungaji Peter akaenda zake kulala


“Bado kichwa changu kinazunguka kuhusu nani aliyenifanyia hivi? Nani ametaka niozee gerezani na kwa nini? Kama kuna mtu niliyemkosea kwa nini asingenifuata tukazungumza kuliko kunifanyia ukatili mkubwa namna hii?Siilaumu mahakama.Simlaumu jaji aliyetoa hukumu .Yawezekana anafahamu kabisa kwamba sikutenda kosa lakini upande wa mashitaka umejitahidi kuishawishi mahakama ikubali nimetenda kosa na hata kama mimi ningetoa hukumu kama


aliyoitoa kutokana na ushahidi uliokuwepo” akawaza Gosu Gous


“Aliyelitengeneza jambo hili alikuwa amejiandaa na lazima ametumia gharama kubwa sana kuhakikisha ninaishia gerezani lakini kwa nini? Hapo ndipo ninapokwama kila ninapolitafakari jambo hili” akawaza Gosu Gosu


DAR ES SALAAM


Ni moja ya siku mbaya sana kwa Ruby mke wa Rais


mstaafu wa Tanzania Dr Fabian Kelelo.Toka mchana alipopata taarifa za Gosu Gosu kuhukumiwa kifungo cha maisha gerezani alijifungia chumbani kwake akilia.


Hali ilikuwa ni ya ukimya mkubwa katika makazi haya ya Rais mstaafu.Dr Fabian akaingia chumbani akiwa amebeba sinia la chakula akaliweka katika meza ndogo,akaisogeza karibu na kitanda kisha taratibu akamshika bega


“Ruby, tafadhali amka ule chakula mke


wangu.Nimeambiwa toka mchana hujaweka kitu chochote tumboni” akasema Dr Fabian


“I have to punish myself ! akasema Ruby


“Kwa nini Ruby? Tafadhali usijitese mpenzi wangu” akasema Dr Fabian


“Rafiki yangu,mtu wangu wa karibu anaozea gerezani na hakuna kitu chochote nilichofanya kumsaidia.Nimebaki kama mtazamaji nikimuona Gosu Gosu anavyopotelea gerezani.I


swear I won’t forgive myself for this !


“My love there is nothing you could’ve done to save him” akasema Dr Fabian


“Afadhali ungeniacha nikamtembelee mahabusu hata mara moja”


“Isingeleta picha nzuri kwetu.Wewe ni mke wa Rais mstaafu isingependeza kwetu kuonyesha tuna ukaribu na mtuhumwa wa mauaji na hata kumtembelea gerezani.Unadhani jamii ingetuchukuliaje? Akasema Dr Fabian


“Gosu Gosu si tu ni mtu wangu wa karibu ninamuhesabu kama ndugu yangu lakini alipopata matatizo nikajitenga naye.Inaniumiza sana Fabian ! akasema Ruby


“Ruby ninafahamu Gosu Gosu ni mtu wa karibu sana nawe na hata mimi pia ni rafiki yangu na ninamuheshimu sana kwani ana mchango wake mkubwa katika usalama wa nchi hii lakini kesi aliyokuwa nayo ni mbaya” akasema Dr Fabian


“You could’ve done something ! akafoka Ruby


“Ruby hakuna chochote ambacho ningeweza kukifanya kumsaidia Gosu Gosu.Kama nilivyokwambia kwamba kesi iliyokuwa inamkabili Gosu Gosu ni mbaya.Nimejaribu kuzungumza hata na mawakili waliokuwa wanamtetea na wakakiri kwamba kesi imemkalia vibaya Gosu Gosu kwani kuna kila ushahidi unaoonyesha kwamba alitenda kosa la mauaji”


“Ninamfahamu Gosu Gosu hawezi akamuua Yule mwanamke ! akasema Ruby


“Gosu Gosu is a killer Ruby ! Hata ukimtazama macho yake yanaonyesha ni muuaji” akasema Dr Fabian


“I know but he wont kill a woman ! Ninamfahamu vizuri Gosu Gosu zaidi ya unavyomfahamu wewe.Nina uhakika mkubwa kwamba hakutenda kosa lile ! akasema Ruby


“Kama si yeye nani aliyefanya mauaji yale? Bastola iliyotumika kufanya mauaji na


ilikutwa eneo la tukio ni ya Gosu Gosu mwenyewe na alikutwa na askari polisi akiwa ameishika mkononi.Bado unaamini kwamba hakutenda kosa? Akauliza Dr Fabian


“I’m confused ! akajibu Ruby


“Sikiliza Ruby.Binafsi nina imani kubwa na mahakama zetu kwamba zinatenda haki na hata katika kesi hii haki imetendeka.Wote tunampenda Gosu Gosu lakini kama ametenda kosa na ametiwa hatiani hakuna chochote tunachoweza kufanya.Lazima


alipe kwa uovu wote alioutenda” akasema Dr Fabian.Ruby akageka nakujilaza hakutaka maongezi tena


GEREZA LA KIMONDO


“Ninafanya kazi ya ulinzi katika kampuni ya ulinzi ya Chemela.Siku tukio la mauji lilipofanyika nilipangiwa kulinda katika hoteli ya kitalii ya Kobe ambako nilipangiwa kulinda mojawapo ya nyumba ya wageni.Nilimpokea lindo


mwenzangu aliyekuwa zamu ya usiku.Mida ya saa Saa tatu hivi mlango wa nyumba ile ukafunguliwa na akatoka mwanaume mmoja akiwa amechafuka damu na mkononi akiwa ameshika bastola akaninyoshea akaniuliza kama kuna mtu yeyote ameingia mle ndani lakini sikuwa nimeona mtu yeyote akiingia mle ndani.Aliniacha na kurejea ndani ndipo nikatoa taarifa haraka kwa wakubwa wangu nao wakawasiliana na polisi


waliofika haraka na kumkamata mtuhumiwa”


“Ndugu Mollel unaweza ukamtambua hapa mahakamani mtu uliyemuona akitoka ndani ya nyumba uliyokuwa ukilinda akiwa amechafuka damu na mkononi akiwa na bastola?


Akauliza wakili na Yule mlinzi akanyoosha kidole kumuelekezea Gosu Gosu


Gosu Gosu akakurupuka kutoka usingizini.Alikuwa anaota akikumbuka mahakamani wakati mashahidi wa upande wa


mashitaka wakitoa ushahidi wao na shahidi wa kwanza kabisa ni mlinzi aliyekuwa analinda nyumba ile waliyokuwa wamefikia Gosu Gosu na Lidya.


“Kumbu kumbu hii itanitesa kwa muda mrefu sana.Ni kweli nilitoka nje ya ile nyumba na bastola nikiwa nimechafuka damu.Sikujua kama nilikuwa najiangamiza mimi mwenyewe.Nilifanya kosa kuishika ile bastola.Nilikuwa nimechanganyikiwa sikujua nilichokuwa nakifanya”


akawaza Gosu Gosu na kukumbuka namna shahidi wa nne ambaye ni askari polisi alivyotoa ushahidi wake mahakamani kuhusiana na ile bastola


“Bastola iliyotumika katika mauaji yale ambayo ilikutwa eneo la tukio inamilikiwa kihalali na mtuhumiwa ambaye ni Papi Gosu Gosu”


“Ushahidi huu uliniangamiza.Ni kweli bastola ile ni ya kwangu na ilitumika katika kumuua Lidya.Swali ambalo mpaka leo sijapata jibu


ni je ilifikaje pale na kufanya mauaji? Nakumbuka niliiacha Dar es salaam katika kasiki langu lakini nikaikuta Arusha.Jambo hili waweza dhani ni kiini macho lakini ni jambo la kweli kabisa.Ni mimi peke yangu ninaye fahamu namba za kufungulia kasiki.Hili jambo ni pana.Inahitaji utulivu wa kutosha kuweza kulichambua.Laiti Mathew Mulumbi angekuwepo angeweza kunisaidia kufanya uchunguzi wa jambo hili na kuubaini ukweli lakini hayupo


na sijui mahala alipo.Zaidi ya miaka mitatu sijawahi kuwasiliana naye.Ruby nilitegemea angeweza kuwa na msaada kwangu lakini imekuwa tofauti kabisa.Toka masahibu haya yamenikuta sijawahi kumuona mahakamani au hata kunitembelea mahabusu.Hajui kama nina kabiliwa na kesi?


Hata kama mawakili wangu wakikata rufaa hakutakuwa na msaada wowote.Utakuwa ni kupoteza muda na fedha kwani ushahidi uko wazi kabisa kwamba nilimuua Lidya.Kitu


cha msingi ambacho kinaweza kunisaidia ni kutafuta nani walionifanyia jambo hili lakini nani anayeweza kuifanya kazi hiyo? Nimepoteza marafiki wote na uchunguzi wa jambo hili unapaswa kufanywa na nguli katika mambo ya upelelezi.Dah ! Nitaozea gerezani ! akawaza Gosu Gosu.


“Mchungaji Peter alikuwa sahihi kuwa nimuachie Mungu atanisaidia” akawaza na kuanza tena kuutafuta usingizi


OKINAWA – JAPAN


Kijiji cha Ogimi kinapatikana katika wilaya ya Kunigami Kaskazini ya kisiwa cha Okinawa nchini Japan.Ni asubuhi familia ya mzee Kohaku Akasaki ikiwa mezani wakipata kifungua kinywa mara wakasikia honi ya gari.Mke wa mzee Kohaku akainuka kwenda kuangalia mtu aliyekuwa amefika asubuhi ile.Baada ya muda akarejea akiwa ameongozana na maafisa wa uhamiaji.Mzee Kohaku akawakaribisha


maafisa wale sebuleni kwa ajili ya mazungumzo


“Tumekuja kuzungumza na Mathew Mulumbi kumkumbusha kwamba kibali chake cha ukaazi kinakaribia kumalizika hivyo anapaswa aanze taratibu za kuomba kibali kingine kam aatapenda kuendelea kukaa hapa” akasema mmoja wa maafisha wale wa uhamiaji.Baada ya mazungumzo ya muda mfupi maafisa wale wakaondoka


Saa moja baada ya wale maafisa wa uhamiaji kuondoka Mathew Mulumbi aliyekuwa


ametoka katika mazoezi ya kukimbia akarejea nyumbani.Ni kawaida yake kukimbia kila siku asubuhi.Mara tu alipowasili akajulishwa kuhusu ujio wa wale maafisa wa uhamiaji.Baada ya kupata kifungua kinywa Mathew akaenda kupumzika ufukweni.Alisalimianana watu kadhaa kisha akatafuta sehemu nzuri akaenda kujilaza mchangani


“Nimeyapenda sana maisha ya hapa Okinawa.Nimejifunza mambo


mengi kutoka kwa watu wa hapa.Ninajiona kama vile niko nyumbani Tanzania kwani ukarimu wa watu wa hapa ni sawa na ule wa watanzania” akawaza Mathew na kustuka baada ya kuwaona watu wakielekea mahala alipokuwa amelala.Alipatwa na mshangao mkubwa baada ya kumuona kijana mmoja anayejishughlisha na uvuvi akiwa ameongozana na mwanamke mwafrika.


“Ni mara ya kwanza toka nimefika hapa kijijini ninamuona mtu


mweusi.Mwafrika niliyepo hapa kijiji ni mimi peke yangu.Huyu katokea wapi?


Akajiuliza Mathew


“Mathew ! akaita Sakahilo na Mathew akasimama


“Mathew nimekuletea mgeni anatokea Afrika.Nimemwambia kuna mwafrika tunaishi naye hapa hakuamini akataka kuonana nawe” akasema Sakahilo.Huku akitabasamu Mathew akampa mkono Yule mwanamke akamsalimu kwa kiingereza


“Unatokea Afrika?


Akauliza Mathew


“Ndiyo ninatokea afrika kusini”


“Sawubona”akasema Mathew huku akitabasamu


“Sanibonani” akajibu Yule mwanamke huku akitabasamu “Unjani? Akauliza Mathew


“Ngisaphila,wena unjani? Akajibu Yule mwanamke huku akicheka


“Ngubani igama lakho?(Jina lako nani?) akauliza Mathew


“Igama lami ngu Sindisiwe.(Jina langu Sindisiwe)


“ Hautajali nikikuita Sindi? Akauliza Mathew


“Wengi wananiita hivyo.Wewe jina lako nani?


“Naitwa Mathew” “Unatokea Afrika kusini


pia? Akauliza Sindi “Hapana ninatokea


Tanzania”Mathew akajibu “Tanzania?! Sindi


akashagaa


“Ndiyo nimetokea Tanzania mbona umeshangaa?


Mathew akauliza


“NI kwa sababu umeweza kuzungumza lugha yetu ya kizulu kama vile nawe


unatokea Afrika kusini” akasema Sindi


“Nimewahi kuishi nchini Afrika kusini kwa muda wa miezi mitatu hivyo nilijifunza kizulu.Lugha zetu za kiafrika zina utamu wake ukizizungumza hasa ukiwa huku ugenini” akasema Mathew na Sindi aliyekuwa amevaa kaptura nyeupe fulana nyeupe na kofia pana ya mduara ya rangi nyeupe akatoa tabasamu pana sana.


“Sindi kama hutajali tuhame mahala hapa tukatafute sehemu nzuri tukae


tuzungumze,tufahamiane vyema”akasema Mathew


“Sawa hakuna tatizo” akajibu Sindi na Mathew akamuongoza katika sehemu nzuri kulikokuwa na maporomoko ya maji na mandhari ya kuvutia


“Wow ! mandhari ya aina yake hii.Nimeipenda sana” akasema Sindi akiifurahia mandhari ile ya kuvutia mno.Mathew akampeleka mahala kulikowekwa viti vya mapumziko wakaketi


“Lazima nikiri nimekipenda kisiwa hiki.Kina


mvuto wa aina yake” akasema Sindi


“Kisiwa hiki cha Okinawa kinatajwa kuwa ni mojawapo ya mahala ambako watu huishi kwa muda mrefu zaidi duniani.Wastani wa umri wa kuishi hapa ni kuanzia miaka themanini.Kisiwa hiki ni mojawapo ya sehemu zinazotajwa kuwa na watu wengi wenye zaidi ya miaka mia moja kuliko sehemu nyingine duniani.Mahala nikakoishi,mzee Kohaku Akasaki ana miaka tisini na tatu na mkewe ana miaka


themanini na moja lakini bado wana afya njema kabisa na nguvu za kutosha.Kule kwetu Afrika au sehemu nyingine duniani mtu wa umri huo anakuwa amechoka sana na yawezekana asiweze hata kutembea lakini wazee hawa wanafanya kazi zao za shambani kama kawaida bila tatizo lolote.Ni nadra sana kusikia magonjwa ya moyo au saratani katika kisiwa hiki” akasema Mathew


“Nini siri yao ya kuishi umri mrefu namna hii?


Akauliza Sindi


“Kwa mujibu wa mtafiti mmoja Profesa Craig Willcox aliyefanya utafiti katika kisiwa hiki kutafuta kwa nini watu wa kisiwa hiki wanaishi kwa miaka mingi anadai kuna sababu za kijenetiki.Lakini si kigezo hicho pekee bali mfumo mzima wa maisha ya hapa.Wanazo huduma bora kabisa za afya,kingine ni chakula wanachokula.Watu wa kisiwa hiki bado wanatumia vyakula vyao vya asili.Asilimia sabini ya chakula cha watu wa hapa ni viazi vitamu ambavyo kule kwenu mnaviita


ubhatata.” Akasema Mathew na Sindi akacheka


“Mathew umenikumbusha nyumbani” akasema Sindi


“Vyakula vingine wanavyotumia kwa kiasi kikubwa ni vile vitokanavyo na nafaka,pia kuna mboga mboga,matunda nk.Sababu nyingine ambayo inachangia kwa watu wa kisiwa hiki kuishi maisha marefu inatajwa kuwa ni ya kimazingira.Kama unavyojionea wewe mwenyewe wamejitahidi mno katika uhifadhi wa mazingira.Kuna uasili mkubwa sana mahala


hapa.Hakuna uchafuzi wa mkubwa wa hewa kwani viwanda ni vichache vilevile magari.Sababu nyingine ni uchapakazi na kuishi maisha yaliyojaa furaha.Nilikwambia kwamba mzee Kohaku Akasaki ninayeishi kwake ana umri wa zaidi ya miaka tisini lakini anafanya kazi zake kama ana miaka hamsini.Analima


,anapanda miti,anafanya mazoezi na kila kitu ambacho mwenye wa miaka hamsini angeweza kufanya.Kwa uchache tu hizo ni sababu zinazowafanya watu wa kisiwa


hiki waishi maisha marefu tofauti na wengine” akasema Mathew


“Ahsante sana Mathew kwa ufafanuzi huo.Nimepata picha pana kwa sasa kuhusiana na kisiwa hiki” akasema Sindi


“Umekuja kufanya utalii?


Ni nadra sana kwa watu wa kutoka Afrika kufika katika kisiwa hiki kufanya utalii”


Akauliza Mathew “Nimekuja kwa jambo


lingine japo hata kufika tu hapa ni sehemu ya utalii.Mimi ni mwigizaji na nimekuja hapa


na timu yangu tunarekodi filamu na katika filamu hiyo mimi ni muhusika mkuu” akasema Sindi


“Hongera.Inaitwaje filamu mnayoicheza? Mathew akauliza


“Inaitwa before I die.NIhadithi inayomuhusu binti mdogo bilionea ambaye maisha yake yalitawaliwa na mauza uza mengi.Filamu hii inatokana na kitabu kilichoandikwa na mwandishi mmoja wa riwaya anatokea Tanzania chenye jina hilo la Before I die”


“Ouh kumbe mwandishi wa hadithi hiyo anatokea Tanzania?! Mathew akashangaa


“Ndiyo anatokea Tanzania.Kampuni ninayofanya nayo kazi imeamua kuwekeza barani Afrika na kuwatumia waandishi na wahusika kutoka Afrika”


“Ni jambo zuri sana kuwainua waafrika katika filamu,lakini imekuaje mkafika hapa?


“Ni kutokana na hadithi yenyewe ilivyo.Tulifanya


mabadiliko kidogo katika hadithi hiyo na hivyo kutulazimu kuja kurekodi kipande cha filamu katika kisiwa hiki lakini kwa asilimia tisini filamu hiyo imechezwa katika mazingira ya Afrika hasa Tanzania”


“Nimefurahi sana kwa taarifa hii.Mtakuwa hapa Okinawa kwa muda gani?


“Hapa hatukai sana kwani sehemu tunayorekodi ni ndogo na maandalizi yote yamekamilika .Tukimaliza kurekodi kipande hicho tutaondoka na kwenda


kumalizia kipande cha mwisho nchini Tanzania”akasema Sindi


“Hiyo ni filamu ambayo sitaki kuikosa pindi itakapotoka” akasema Mathew


“Tayari matangazo yake yamekwisha anza kutoka na kwa tathimi iliyofanywa inaonekana ni filamu ambayo itakuwa na mauzo makubwa.Wewe unafanya nini huku? Sikutegemea kabisa kama ningeweza kukutana mahala hapa na mtu anayetokea Afrika.Nilipoambiwa kwamba


kuna mwafrika hapa Ogimi nilikataa ndipo yule jamaa akanileta kwako.Mathew unafahamika sana hapa Ogimi”


“Niko mwafrika peke yangu hapa Ogimi hivyo ni rahisi sana kujulikana.Kwa ujumla watu wa hapa wananipenda sana nami nawapenda.Wengi wananifahamu na wananichukulia kama mwenzao.Sijawahi kubaguliwa”


“Nini unakifanya hapa?


“Hapa nimekuja kupumzika”


“Kupumzika? Sindi akaonekana kushangaa


“Ndiyo nimekuja kupumzika”


“Kwa nini ukachagua mahala hapa? Kuna sehemu nyingi barani Afrika ambazo ungeweza kupumzika.Ungeweza kwenda Zanzibar,ungeweza kwenda katika nchi yoyote ya kiafrika kupumzika lakini ukachagua kuja hapa”


“Nilichagua sehemu ya mbali kabisa ambako hakuna


mtu anayenifahamu ndiyo maana nikafika hapa”Mathew akajibu


“Kwani umekaa hapa kwa muda gani?


“Nina zaidi ya miaka mitatu”


“Miaka mitatu? Sindi akazidi kushangaa


“Ndiyo nina zaidi ya miaka mitatu mahala hapa”


“Miaka hiyo mitatu unapumzika tu au kuna kitu unakimbia huko ulikotoka?


Akauliza Sindi


“Sikupanga kukaa hapa muda mrefu kiasi hicho lakini


kutokana na upendo wa watu wa hapa kila pale muda wangu wa ukaazi unapoisha ninajikuta nikiongeza tena muda”


“Unamudu vipi gharama za kuishi hapa kwa muda huo wote wa miaka mitatu? Kuna kazi unafanya ya kuingiza kipato?


“Hakuna kazi ninafanya.Nimekwambia watu wa hapa ni wakarimu sana.Bwana na bi Kohaku Akasaki wananitunza kama mtoto wao.Ni upendo mkubwa sana.Wamenifanya niijione


niko nyumbani kwani watanzania pia tuna upendo wa namna hii kwa wageni ndiyo maana kila mgeni anayetembelea Tanzania haachi kuzungumzia upendo wa watu wake”akasema Mathew


“Uko sahihi Mathew.Watanzania wamebarikiwa upendo na ukarimu wa kipekee kabisa naweza kusema kuliko wote barani Afrika.Tumekuwa Tanzania tunarekodi filamu yetu na kila mmoja anashangaa kwa upendo na


ukarimu wa ajabu tunaoonyeshwa na wenyeji wetu.Ninyi ni wa kipekee kabisa natamani na watu wa Afrika Kusini wangekuwa na upendo wa namna hiyo hasa kwa wageni lakini badala yake wageni hasa wa kutoka nchi za Afrika hawatakiwi nchini kwetu” akasema Sindi kwa masikitiko


“Hili jambo limeleta aibu kubwa sana kwa nchi ya Afrika kusini.Kitendo cha kuwabagua waafrika wenzao kimeishangaza dunia.Nilikuwa nafuatilia katika runinga


vurugu zilizotokea nchini Afrika kusini wazawa wakiwafukuza wahamiaji kutoka mataifa mengine ya kiafrika,wanachoma mali na biashara zao na wakati mwingine hata kuwaua wageni.Nini sababu ya kufanya hivi?Kwa nini kumekuwa na chuki kubwa dhidi ya wageni hasa wale wanaotoka katika mataifa ya afrika? Akauliza Mathew


“Suala hili ni pana sana Mathew na sijui nilieleze vipi kwani limekusanya mambo mengi ndani yake.Makundi ya


watu wanaoendesha matendo hayo ambao wengi wao ni vijana,wanadai kwamba wageni wengi wanaoingia nchini mwao wanachukua fursa zao za ajira na wengi wa wahamiaji hawa huingia kinyemela bila kuwa na vibali.Zipo vile vile sababu za kisiasa n.k”


“Sindi nafahamu jambo hili ni pana lakini linastahili kukemewa na kulaaniwa kwa nguvu zote kwani linabomoa ule umoja wa Afrika ambao ulihimizwa na waasisi wa mataifa yetu ambao walipenda


sana kuiona Afrika ikiwa moja.Tazama kwa hiki kilichotokea mahusiano kati ya Afrika kusini na nchi nyingine za kiafrika yameingia dosari.Unadhani raia wa Afrika kusini ataonekanaje nchini Nigeria? Ni wazi kutakuwa na uhasama mkubwa miongoni mwa waafrika na hii itawachafua raia wote wa Afrika kusini kila watakapoonekana katika bara la Afrika watachukuliwa ni wabaguzi”


“Nakubaliana nawe Mathew kwamba hili jambo


limetia aibua nchi ya Afrika kusini na vile vile limepunguza juhudi za kuifanya Afrika kuwa moja.Sioni sababu ya kubaguana sisi kwa sisi.Waasisi wa mataifa yetu akina mzee Julius Nyerere,Mzee Mandela,Mugabe,Muammar Gaddafi na wengineo jambo hili litakuwa linawaumiza mno huko waliko.Lakini Mathew kitu cha kushangaza kuhusu vurugu hizi ni kwamba hata maduka yanayomilikiwa na wazawa nayo pia yanachomwa na kuporwa.Nadhani elimu


kubwa inatakiwa kwa raia wa Afrika kusini ili wawaone waafrika wenzao ni sawa na wao.Bara la Afrika lilisimama na wao katika harakati za ukombozi lakini leo hii nadhani historia hiyo wamekwisha isahau.Kuna umuhimu wa kuwakumbusha kwamba sisi pia tuliishi katika nchi za wengine kama wahamiaji na hatukufukuzwa wala kubaguliwa.Watu wetu walioishi katika mataifa ya Afrika wakitafuta uhuru hawakuitwa wahamiaji bali wapigania uhuru”


“Sawa kabisa.Hadi leo hii nchini Tanzania kuna kumbu kumbu ya makaburi ya wapigania uhuru.Hawafundishwi mashuleni nchi yenu ilikotoka?


Mathew akauliza


“Upo ulazima mkubwa wa kutoa elimu kubwa sana hasa kwa kizazi cha sasa.Mathew tuachane na masuala hayo yanayotufanya waafrika tudharaulike kila mahala tunakopita duniani.Lini unarejea nyumbani? Akauliza Sindi


“Kibali changu cha ukaazi kinakaribia kumalizika.Nimekata shauri sintaomba tena kuendelea kukaa hapa nitarejea nyumbani nikaungane na wenzangu kuijenga nchi yetu” akasema Mathew


“Unajishughulisha na nini nchini Tanzania? Akauliza Sindi


“Nina vibiashara kidogo pia nina mashamba na mifugo michache”


“Familia yako mnawasiliana?


“Ndiyo tunawasiliana”


“Una watoto wangapi? “Nina watoto wanne” “Wanne?! Akauliza Sindi


akionekana kushangaa “Mbona umeshangaa Sindi


kuwa na watoto wanne?


Akauliza Mathew “Nimeshangaa kidogo kwa


kuwa vijana wengi wa zama hizi hupenda kuwa na mtoto mmoja au wawili” akasema Sindi


“Hayo ni mambo ya kuiga kutoka kwa wageni.Mungu ametuleta hapa tuijaze dunia na bado haijajaa.Tunapojaliwa uwezo wa kupata watoto


tuutumie kwani wako mamia ya watu ambao wanahangaika usiku na mchana kutafuta watoto na wanamlilia Mungu awajalie hata mtoto mmoja.Vipi wewe una watoto wangapi? Akauliza Mathew na Sindi akacheka


“Mpaka sasa bado sijapata mtoto” akasema Sindi


“Unasubiri nini? Tatizo lenu ninyi wanawake warembo na hasa ninyi wenye majina mnaogopa sana kupata watoto.Wengi mnahofia maumbo yenu kubadilika na kupoteza ule mvuto wa awali


na wengine wanahofia kazi ya ulezi wa mtoto.Msidanganywe kwamba mkipata watoto maumbo yenu yatabadilika” akasema Mathew na wote wakaangua kicheko.Maongezi ya ya Mathew na Sindi yalikuwa matamu na mara Sindi akakumbuka kwamba anahitaji kurudi kwa wenzake


“Mathew imekuwa ni furaha kubwa kukutana nawe mahala hapa.Ni jambo ambalo sikulitegemea kabisa”


“Mimi pia sikutegemeakama ningekutana na mwafrika mwenzangu


mahala hapa” akasema Mathew na Sindi akamjulisha kwamba anahitaji kurejea katika kambi yao.Mathew akamsindikiza kuelekea katika kambi yao huku wakizungumza kwa furaha.Wakati wakielekea katika kambi ya akina Sindi,wakakutana na bibi mmoja anayejulikana kama bibi Hinata ambaye ana sifa kubwa ya utabiri.Bibi Hinata alipowaona akina Mathew akawaita wakamsalimu akawataka waketi.Bibi Hinata akamtaka Mathew


amuonyeshe viganja vyake vya mkono.Akavishika na kufumba macho halafu akasema


“Wewe ni jasiri,shujaa,usiyeogopa kitu chochote.Wewe ni msaada mkubwa kwa watu,nenda nyumbani kawasaidie watu wako”


Maneno yale ya bi Hinata yalimsisimua sana Mathew.Akamtazama Yule bibi na kumshukuru kwa maneno yake akampatia fedha kidogo


“Yule bibi ni nani?


Akauliza Sindi


“Yule bibi anaheshimika sana hapa Ogimi.Anafahamika kwa uwezo wake mkubwa katika kutabiri mambo.Kwa kule kwenu mnawaita umbhuli.Akitazama viganja vyako vya mikono anaweza akafahamu wewe ni nani na unafanya nini na anaweza akakutabiria hata mambo ya mbeleni” akasema Mathew


“Maneno yale kwamba wewe ni jasiri,shujaa usiyeogopa kitu ni ya kweli?


Akauliza Sindi “Sifahamu alikuwa


anamaanisha nini kwa maneno


yale” akasema Mathew na safari ikaendelea hadi walipofika katika kambi ya akina Sindi wakaagana kwa miadi ya kuonana siku inayofuata.


“Nimefurahi mno siku ya leo kukutana na Sindi.Kwa miaka mitatu nimekuwa mwafrika peke yangu katika kisiwa hiki.Amenipa hamu ya kurejea haraka nyumbani” akawaza Mathew na mara akayakumbuka maneno ya bibi Hinata


“Mimi si muumini sana wa haya mambo ya utabiri lakini


bibi Hinata ametamka maneno ambayo yamejaa ukweli mtupu.Hinata amemalizia maelezo yake kwa kusema kwamba natakiwa niende nyumbani nikawasaidie watu wangu kuna kitu chochote alikimaanisha? Bibi yule ni maarufu na anaheshimika sana kwa kazi yake anayoifanya ya utabiri sitakiwi kumpuuza.Nadhani ni muda mufaka wa kurejea nyumbani.Nimekaa hapa kwa muda wa zaidi ya miaka mitatu na hakuna mtu wangu yeyote anayefahamu mahala


nilipo.Yawezekana wengine tayari wanahisi nimekwisha fariki kumbe bado ni mzima wa afya.Nilikuja hapa kwa ajili ya kujitafakari kuhusu maisha yangu.Nilihitaji kupata muda wa kutosha wa kuyatafakari maisha yangu na kwa sasa niko tayari kukabiliana tena na maisha yangu.Nimekubali siwezi kuwa na maisha ya kawaida kama watu wengine,misuko suki imekuwa ni sehemu ya maisha yangu hivyo lazima niwe tayari kukabiliana nayo.Nimegundua kwamba sikuingia katika kazi


ya ujasusi kwa bahati mbaya.Nimeingia katika kazi hii kwa malengo maalum.Mungu ananitumia katika kuipigania nchi yangu na ndiyo maana nimeweza kufanikiwa kugundua mambo mengine magumu kabisa na mengine yakiwa ni siri kubwa.Kila mtu hapa duniani ana kusudi lake la kuwepo hapa,mimi nimelitambua jukumu langu na sipaswi kulikimbia.Bibi Hinata alisema mimi ni shujaa nisiyeogopa kitu hivyo napaswa kurejea nyumbani kusaidia watu


wangu” akawaza Mathew wakati akielekea nyumbani


GEREZA LA KIMONDO – ARUSHA TANZANIA


Saa kumi na mbili za alfajiri,kililia king’ora na wafungwa wote wakaamka wakaenda kujipanga kwa ajili ya kazi za usafi wa gereza kwa asubuhi ile.Gosu Gosu alikuwa na adhabu ya kudeki vyoo kumi na saba na mabafu ishirini na mbili kutokana kutokana na kosa la kupigana usiku uliotangulia.Alipelekwa


sehemu anakotakiwa kufanya usafi akapewa vifaa akasimama akavitazama vile vifaa


“Naomba Mungu anioteshe hata kwenye ndoto sura ya mtu aliyenifanyia jambo hili?Kwa nini nateseka kwa jambo ambalo sikulitenda? Akawaza Gosu Gosu na askari magereza aliyekuwa akimsimamia akamsogelea.


“Huyu askari naye asithubutu kunikorofisha hasira zangu zote zitaishia kwake” akawaza Gosu Gosu.


“Kaka mbona huanzi usafi? Jitahidi kabla king’ora cha kifungua kinywa hakijalia uwe umemaliza” akasema Yule askari na Gosu Gosu akachukua ufagio akaanza kudeki


“Samahani Afande” akasema Gosu Gosu


“Unasemaje?


“Wale jamaa niliopigana nao jana usiku wamepewa adhabu gani?Mbona adhabu nimepewa peke yangu?


“Sikuwepo jana usiku hivyo siwezi kufahamu kilichotokea hapa


gerezani.Nimekuja asubuhi hii na kupangiwa kusimamia usafi wa vyoo” akajibu Yule askari na Gosu Gosu hakutaka maongezi akaendelea na usafi


“Namwachia Mungu atanilipia kwani yeye anafahamu sikutenda kosa la mauaji na hapa ninatumikia adhabu aliyostahili mtu mwingine kabisa” akaendelea kuwaza Gosu Gosu


Wakati akiendelea na usafi wa choo mara wakatokea watu wanne wakasimama mlangoni mwa choo alichokuwa anadeki.Gosu Gosu akaacha


kazi aliyokuwa anaifanya akageuka akakutana na sura zile zile za jana usiku katika bwalo la chakula.Sura ya Gosu Gosu ikabadilika akapandwa na hasira


“Malaika wangu anisimamie kwa hiki nitakachowafanya hawa jamaa” akawaza Gosu Gosu


“Tumekutana tena.Leo tunataka tukuonyeshe nani mkuu hapa gerezani” akasema Yule jamaa mfupi mweusi ambaye alikuwa na plasta usoni kutokana na kipigo alichopewa usiku.Jamaa


watatu waliingia mle chooni na kila mmoja akatoa kisu halafu yulejamaa mweusi akawapa ishara wale jamaa wawili aliokuwa nao mle chooni wamsogelee Gosu Gosu wakiwa na visu.


“Kitu gani mnahitaji kwangu? Akauliza Gosu Gosu


“Haraka haraka mvueni suruali tumfunze adabu ! Jana ulipata bahati wakafika askari kukuokoa leo hii hakuna atakayekuja kukuokoa.Utajuta kilichokuleta hapa gerezani ! akasema Yule jamaa mfupi.Wale jamaa wawili


wakazidi kumkaribia Gosu Gosu.


“Hawa jamaa wanatafuta kufia katika mikono yangu ! akawaza Gosu Gosu na kwa haraka akauvunja mti wa ufagio ule mkubwa aliokuwa anautumia kudeki choo halafu akawatandika usoni wale jamaa wawili kwa kutumia vipande viwili alivyokuwa amevishika mikononi.Akamuwahi jamaa mmoja akamkamata kichwa na kukigongesha katika goti lake mara mbili.Yule jamaa mfupi akaruka akiwa na kisu


mkononi kwa ajili ya kumchoma nacho Gosu Gosu lakini alikiwsha muona akakinga mkono na kisu kile kikachoma mkono karibu na kiwiko.Kwa hasira Gosu Gosu akaudaka mkono wa Yule jamaa kwa mikono yake miwili halafu akaupiga katika goti lake na sauti ya mvunjiko wa kitu kigumu ikasikika.Mkono wa Yule jamaa ulikuwa umevunjiika.


“Aaaaghh !! akapiga kelele Yule jamaa Gosu Gosu hakumjali akamsogeza karibu na kumtandika kichwa kizito


akaanguka chini.Akamfuata chini na kuanza kumvurumishia magumi.Pembeni ya Yule jamaa akakiona kisu akakiokota lakini wakaingia watu wengine wawili mle chooni na mapigano yakaendelea.


“Leo nitawafunza adabu wajinga nyie !! akasema kwa hasira Gosu Gosu na kuendelea kutembeza kipigo kwa wale jamaa mle ndani.Alikuwa anavuja damu kutokana na kuchomwa na visu sehemu mbali mbali za


mwili wake lakini na wale jamaa hakuna aliyekuwa anatembea.Wote walikuwa chini wakilia kwa maumivu makali,karibu wote walikuwa wamevunjwa miguu na wengine mikono


“Nadhani sasa adabu itakuja.Siku nyingine mkinifuata nitawachinja ! akasema Gosu Gosu huku akiendelea kumvurumishia magumi Yule jamaa mfupi licha ya kuwa tayari amekwisha mvunja mikono yote miwili.Mara wakaingia askari magereza na Gosu Gosu


akakamatwa akapelekwa zahanati kwa ajili ya kugangwa sehemu zile alizokuwa amechomwa visu na wale jamaa halafu akapelekwa katika mahabusu ya gereza.


“Inaonekana hapa katika hili gereza kuna watu ambao wanaruhusiwa kufanya kitu chochote au hata kuua pasi na kuchukuliwa hatua yoyte.Kama ningekuwa lege lege wale jamaa wangeweza hata kuniua.Kinachoshangaza baada ya wale jamaa kutokea hata Yule askari aliyekuwa ananisimamia katika usafi


alitoweka na hii inanipa picha kwamba walilibariki tukio lile.Kwa nini wanaruhusu mfungwa atembee na kisu gerezani? Naona maisha yangu hapa yatakuwa magumu sana.Matukio kama haya yataendelea kutokea tena na tena na ninahisi labda nimeletwa hapa makusudi ili niuawe.Nimekwisha kuona dalili mbaya hapa.Kwanza jana usiku nimechokozwa tukapigana lakini nikaadhibiwa peke yangu.Naamini kuanzia sasa nitaandamwa sana lakini


nitasimama imara sintakubali mtu anionee nitawabadili sura zao hawanifahamu vizuri.Mimi ni mtu mbaya sana na hiki nilichowafanyia leo ni salamu tu” akawaza Gosu Gosu akiwa katika mahabusu ya gereza


“Bado nitaendelea kumlaani mtu mtu aliyenifanyia hivi.Nimemkosea kitu gani? Akaendelea kuwaza Gosu Gosu akiwa amekaa sakafuni


“Nina mkosi na wanawake hawa warembo.Kila ninapokutana na mwanamke na kuanzisha mahusiano


lazima kuna jambo baya litanifika.Nilinusurika kuuawa kwa sababu ya Melanie na sasa kwa sababu ya Lidya ninaozea gerezani.Kama nisingeingia katika mahusiano na Lidya hivi sasa ningekuwa naendelea na maisha yangu vizuri bila matatizo.Lakini siamini kama nina mkosi.Mungu katuumba sawa na mimi ni mwaume rijali kwa nini nisiwe na mahusiano? Akajiuliza Gosu Gosu na picha ya mwili wa Lidya ukiwa umelala katika dimbwi la damu kitandani


ikamjia halafu akastuka baada ya kukumbuka kitu.


“Kuna kitu nimekikumbuka.Nilipotoka kwenda jikoni kuandaa kifungua kinywa nilimuacha Lidya akiwa na kitandani na kompyuta yake lakini baada ya mauaji yale sikuikuta kompyuta ile kitandani au sehemu ya karibu” akawaza Gosu Gosu


“Sasa nimeanza kupata picha.Ni kweli kompyuta ya Lidya haikuwepo mle chumbani.Nakumbuka nilizunguka zunguka mle


chumbani lakini nilikuwa nimechanganyikiwa sikukumbuka kitu kama hiki.Hapa lazima kuna jambo liko nyuma ya tukio hili.Mauaji ya Lidya lazima yana sababu maalum” akawaza Gosu Gosu na kuendelea kuvuta kumbu kumbu ya siku ile yalipotokea mauaji ya Lidya


“Kwa muda wote wa kesi sikuwahi kufikiria kitu kama hiki.Halafu ..oh my God ! akawaza Gosu Gosu na kukumbuka kitu kingine mwili ukamsisimka


“Simu ya Lidya.! Akawaza Gosu Gosu


“Lidya simu zake ilikuwa mezani wakati mimi simu yangu nilikuwa nimeizima na kuiweka katika chaji.Picha ninayoikumbuka simu ya Lidya haikuwepo pale mezani pembeni ya kitanda.Sasa akili yangu imekaa sawa na ndiyo maana nimeanza kukumbuka mambo haya muhimu.Naanza kupata picha kwamba kuna jambo lililopelekea Lidya akauawa na mzigo wote nikaangushiwa mimi.Lidya alikuwa mwandishi wa habari


za uchunguzi naanza kuhisi kuna jambo aliligundua katika uchunguzi wake lililopelekea mauti yake.Niliwahi kumuonya kuhusiana na kazi anayoifanya lakini yeye akasisitiza kwamba ni kazi anayoipenda.Hizi ni habari nzuri sana katika kuanza uchunguzi wa jambo hili lakini nani nitamweleza mambo haya? Ningeweza kumfikishia Ruby taarifa hizi lakini simuamini tena kwani toka nilipopata matatizo haya amepotea na sijawahi kumuona.Hakuna tena


mwingine ninayemuamini anayeweza kunisaidia.Angekuwepo Mathew Mulumbi asingekubali nikaingia gerezani.Mathew Mulumbi ni mtu pekee ambaye anaweza akakubali risasi iliyoelekezwa kwangu impige yeye ili mimi niwe salama.Ee Mungu kama unanisikia muondoe Mathew Mulumbi mahala alipo mrejeshe nyumbani.Ni yeye ambaye anaweza akanisaidia katika jambo hili” akawaza Gosu Gosu


OKINAWA – JAPAN


Saa tano za asubuhi Mathew alitembelea kambi ya akina Sindi akakutana naSindi ambaye alimtambulisha kwa wenzake na wote wakafurahi kwa kukutana na mwafrika mahala pale na hasa anayetokea nchini Tanzania ambako wamerekodi sehemu kubwa ya filamu yao.Sindi alirekodi sehemu yake usiku hivyo mchana ule alikuwa huru akaondoka na Mathew wakaenda kutembea sehemu


mbali mbali za kijiji kile cha Ogimi.


“Sindi mimi nitaondoka hivi karibuni kurejea nyumbani Tanzania” Mathew akamwambia Sindi


“Ouh tena nilitaka kukwambia kwamba nimemaliza kurekodi kipande changu hapa hivyo natakiwa kwenda kumaliza kipande cha mwisho nchini Tanzania.Baada ya viongozi kuridhika na kazi tuliyoifanya hapa basi wameamua tuondoke kesho kurejea Tanzania kwenda kumalizia


sehemu yetu.Kampuni yetu ni kubwa tunayo ndege yetu ambayo itatupeleka kwanza Afrika kusini ambako kuna watu watashuka halafu wengine tutaendelea na safari kuelekea Tanzania.Kwa kuwa nawe unaelekea huko ninaweza kukufanyia mpango ukaongozana nasi na kuokoa pesa ambayo ungeitumia kwa nauli” akasema Sindi


“Hilo litakuwa jambo jema sana Sindi.Nitashukuru kama utanisaidia kwa hilo”akasema Mathew.Siku hii alimzungusha Sindi sehemu


mbali mbali za kisiwa kile cha Okinawa hadi ilipofika jioni walirejea katika kambi ya akina Sindi ambaye aliwaomba wakubwa wake ili Mathew aweze kusafiri nao kuelekea Tanzania na hakukuwa na kipingamizi chochote.


“Ninahisi kama vile kuna nguvu inanirudisha nyumbani.Kwanza ni kufuatwa na maafisa wa uhamiaji kunikumbnusha kwamba kibali changu cha ukaazi kinakaribia kumalizika.Wakati nikijiandaa kuomba kibali kingine mara akatokea Sindi


ambaye baada ya kuonana naye nilijikuta nikipata hamu ya kurejea nyumbani.Kam ahaitoshi nikakutana na bibi Hinata ambaye alinitabiria kwamba natakiwa nikawasaidie watu wangu nyumbani.Si mara ya kwanza kukutana na bibi Yule na hajawahi kunitabiria chochote lakini leo amenitabiria.Ninarudi nyumbani lazima kuna jambo” akawaza Mathew


DAR ES SLAAM – TANZANIA


Ndege inayotumiwa na kampuni kubwa ya filamu ya African pictures yenye makao yake makuu nchini Afrika Kusini ilitua katika uwanja wa ndege wa Julius Nyerere jijini Dar es salaam ikitokea jijini Johannesburg Afrika kusini.Safari ya ndege hii ilianzia nchini Japan ambako wasanii wanaoshiriki katika filamu ya Before I die inayotengenezwa na kampuni hii ya African pictures,walikwenda kurekodi


kipande cha filamu na baada ya kumaliza kurekodi baadhi ya wasanii wakatakiwa kurejea nchini Tanzania ambako wangekwenda kumalizia sehemu ya filamu hiyo


Miongoni mwa watu waliowasili Dar es salaam na ndege hiyo alikuwemo Mathew Mulumbi.


“Hatimaye nimerejea Dar es salaam” akawaza Mathew wakati ndege ikitua.


Ndege ilitua salama na kusimama na maandalizi ya kushuka yakaanza


“Sindi nakushukuru sana kwa msaada huu mkubwa wa usafiri.Nimeokoa kiasi kikubwa cha fedha ambacho ningekitumia kama nauli”


Mathew akamwambia Sindi “Usijali Mathew.Naamini


tutakuwa na wasaa wa kuzungumza hapa Dar es salaam na vile vile ningependa kuzifahamu sehemu mbali mbali za jiji hili na Tanzania kwa ujumla pale nitakapokuwa na nafasi na ningeomba wewe uwe mwenyeji wangu kama hutajali” akasema Sindi


“Usihofu Sindi.Nitakupeleka kokote unakotaka kwenda kutembelea” akasema Mathew kisha akawashukuru viongozi wa msafara ule ambao walimruhusu asafiri nao akawasaidia kushusha vifaa kisha wakaelekea katika jengo la uwanja kwa ajili ya ukaguzi na taratibu nyingine za uhamiaji.


Mambo yalikwenda haraka haraka na watu wote wakaruhusiwa kuingia nchini Tanzania.


“Sindi mimi nitachukua taksi kuelekea katika makazi yangu lakini nakuahidi nitakuja kukutembelea katika kambi yenu kujua unavyoendelea” akasema Mathew akakumbatiana na Sindi kisha akachukua taksi na kumuelekeza dereva ampeleke nyumbani kwake


“Sijui kwa nini kila ninaporejea nchini kutoka ugenini ninajihi amani ya ajabu sana.Nafurahi kurejea nyumbani.This time I’m back for good.Nadhani sasa ni wakati wa kujiwekeza zaidi


hapa nyumbani.Sina mpango tena wa kwenda ng’ambo.Nina biashara zangu ambazo kwa usimamizi wa Gosu Gosu naamini zinakwenda vizuri.Nitashirikiana naye kupanua zaidi biashara zetu” akawaza Mathew akiwa katika taksi akielekea nyumbani kwake.


“Sikutaka kujitambulisha kwa Sindi mimi ni nani.Mara nyingi mimi si mtu wa kujikweza na sipendi kujigamba.Hata hivyo Sindi ni mwanamke mzuri na kuna dalili tutakuwa marafiki


wazuri kadiri muda unavyokwenda japo sitaki kuingianaye katika mahusiano ya kimapenzi” akaendelea kuwaza Mathew.


“Nimemuwaza Sindi nikamkumbuka Ruby.Sina taarifa zake zozote.Sifahamu kama bado atakuwepo hapa Dar es salaam au atakuwa ameondoka.Naamini atakuwa aliumizwa sana na ujumbe niliomtumia kwamba aendelee na maisha yake na asinisubiri.Sijilaumu kwa maamuzi yale ya kumuacha akaendelee na maisha yake


japokuwa naamini ni mwanamke aliyekuwa ananipenda kwa dhati ya moyo wake.Nilihitaji muda wa kujitafakari mimi mwenyewe kuhusu maisha yangu na sikujua ingechukua muda gani kurejea hapa nchini.Isingekuwa haki kumpotezea muda wake mwaname mzuri kama Ruby ndiyo maana nikampa uhuru aendelee na maisha yake.Nitafurahi sana kama atakuwa amepata mwanaume na ameolewa kwani kama angekuwa na mimi angekuwa


akiteseka sana kama ilivyokuwa kwa Peniela” akawaza


Taksi aliyopanda Mathew ilifika nyumbani kwake akamlipa dereva na kushuka.Akasimama akavua miwani myeusi aliyokuwa amevaa akalitazama jumba lake namna lilivyokuwa likionekana kutokea nje.Lilipendeza kwa rangi,miti na maua mazuri yaliyopandwa,akatabasamu na kwenda getini akabonyeza kengele na kusubiri lakini hakuna mtu yeyote aliyetoka


kuja kumfungulia geti.Akabonyeza tena kusubiri hakuna mtu aliyetokea.


“Hakuna watu humu ndani? Akajiuliza Mathew


“Halafu mbona hakuna walinzi hapa getini? Akazidi kushangaa


“Nyumba hii haijawahi kukosa walinzi hata siku moja” akawaza na kwenda katika mlango mdogo wa pembeni akajaribu kuusukuma ukafunguka akaingia ndani.Kulikuwa na ukimya mkubwa.Akaanza kuelekea


ndani huku akiwa na wasi wasi.


“Ukimya huu unanishangaza .Watu wote wako wapi? Au tayari nyumba imeuzwa? Akajiuliza na kwenda hadi katika mlango mkubwa wa sebuleni akajaribu kugonga lakini mlango haukufunguliwa.Akakinyonga kitasa kilikuwa kimefungwa.Akazunguka kwa nyuma nako pia kulikuwa kumefungwa.


“Hellooo ! akaita kwa sauti na mara akasikia mbwa akibweka


“Bravo ! akasema Mathew kwa furaha baada ya kusikia sauti ya mbwa wake ampendaye.Moja kwa moja akaelekea katika banda la mbwa wake akamsemesha maneno Fulani na Bravo mbwa mwenye mafunzo makubwa akalala chini.Mathew kwa furaha akamuwekea mkono kichwani


“I missed you Bravo ! akasema Mathew akiwa mwingi wa furaha baada ya kumuona tena mbwa wake.Akiwa na Bravo mara akasikia hatua za mtu


akageuka akakutanisha macho na kijana mmoja ambaye macho yake yalionekana kutoka usingizini


“Victor ! akasema Mathew “Bosi” akasema Victor kwa


mshangao mkubwa.Mathew akasimama wakakumbatiana “Bosi ni wewe kweli?


Akauliza Victor ambaye ni mfanyakazi wa muda mrefu sana wa Mathew ambaye kazi yake ni kutunza mazingira ya nyumba.Kutokana na kufanya kazi vizuri na kwa muda mrefu Mathew aliamua kumjengea Victor nyumba ndogo ya kuishi


katika makazi yake.Victor alichanganyikiwa alipomuona Mathew hakuamini


“Nimeita sana ulikuwa wapi? Akauliza Mathew


“Utanisamehe bosi nilikuwa nimelala kule ndani na nimestuka baada ya kumsikia Bravo akibweka” akasema Victor kisha akamtaka Mathew amsubiri akakimbia hadi ndani kwake akarejea na ufunguo wa nyumba kubwa na kufungua mlango wa sebuleni


“Karibu bosi” akasema Victor


“Ahsante sana Victor.Watu wote wako wapi humu? Mbona nyumba iko kimya namna hii? Hata walinzi hawaonekani” akasema Mathew lakini Victor hakumjibu


“Watu wote wako wapi Victor? Mbona nyumba hii ni kama vile haijakaliwa na watu kwa miezi kadhaa? Lucy yuko wapi?Akauliza Mathew


“Lucy hayupo tena hapa alipata mume akaolewa na baada ya kuondoka kaka Gosu Gosu hakuajiri tena mtumishi mwingine wa ndani” akasema


Victor na Mathew akatabasamu


“Jambo zuri sana hilo.Utanipa namba zake za simu niwasiliane naye nimpongeze na vile vile kumpatia zawadi.Wewe na Lucy ni watu wangu wa zamani sana hivyo ni sehemu ya ndugu zangu” akasema Mathew


“Hongereni kwa kuitunza vyema nyumba hii.Inapendeza utadhani ni nyumba mpya kumbe ni nyumba ya zamani.Gosu Gosu yuko


kazini? Akauliza Mathew na Victor akasita kidogo kujibu “Yuko wapi Gosu Gosu?


Akauliza Mathew


“Yuko kazini” akajibu Victor


“Yeye anaishi wapi siku hizi?


“Anaishi hapa lakini amekuwa na safari za mara kwa mara kwenda mikoani kikazi.Wamefungua tawi lingine Arusha”


“Ouh kumbe tayari wana tawi lingine Arusha?


“Ndiyo bosi wana tawi lingine Arusha ndiyo maana


Gosu Gosu huwa hakai sana hapa” akajibu Victor


“Vipi kuhusu walinzi kwa nini hakuna walinzi getini?


Akauliza Mathew “Kulitokea mgogoro


kidogo na ile kampuni waliyokuwa wakilinda hapa kaka Gosu Gosu akawaondoa.Anatafuta walinzi wengine” akajibu Victor


“Sawa.Ninakwenda kuoga mpigie simu Gosu Gosu mwambie nimekwisha rejea nahitaji kuonana naye” akasema Mathew na kuelekea


chumbani kwake akimuacha Victor akiwa bado amesimama


“Kama wamefungua tawi lingine Arusha basi maendeleo ya biashara ni mazuri sana.Namkubali Gosu Gosu katika usimamizi wa biashara.Hana mzaha na uzembe wa aina yoyote.Kwa kweli nilipata jembe.Hata kama nikiondoka miaka kumi ninaamini biashara na mali zangu ziko katika mikono salama.Hata hivyo kuna kitu nahisi kama hakiko sawa hapa nyumbani.Hata siku moja hakujawahi kukosekana


walinzi wa kulinda kwani hata Gosu Gosu mwenyew e anafahamu kwamba hapa ndani kuna silaha ninazihifadhi hivyo lazima ulinzi uimarishwe.Lakini nitaonana naye baadae atanieleza kwa nini ameondoa walinzi wote” akawaza Mathew na kufungua mlango wake akaingia ndani.


“Nilikumbuka sana chumba changu” akawaza na kujilaza katika kitanda chake na kuvuta pumzi ndefu


“Home sweet home” akasema halafu akainuka


akaenda bafuni kuoga kisha akavaa nguo za michezo akatoka mle ndani akashuka chini akaenda jikoni akafungua friji lakini hakukuwa na kitu chochote zaidi ya chupa mbili za maji ya kunywa.


“What’s going on here?


Friji ni tupu na inaonekana ina muda mrefu haijawashwa.Si kawaida ya Gosu Gosu kuishi na friji likiwa tupu namna hii.Hakuna kitu anachojali Gosu Gosu kama chakula.Iwezeje friji likose hata tunda moja? Akajiuliza


Mathew na mara akasikia mungurumo wa gari akatoka akijua ni Gosu Gosu amerejea baada ya kupewa taarifa kwamba amerudi lakini akashangaa kukutana na Victor.Alikuwa ametoka kununua vitu mbali mbali supermarket.Mathew akamsaidia kushusha maboksi ya vyakula toka garini na kuingiza jikoni


“Umekwisha mjulisha Gosu Gosu kwamba nimerejea na ninahitaji kumuona?


Akauliza Mathew na Victor akavuta pumzi ndefu


akamtaka Mathew waelekee sebuleni wakazungumze


“Kuna nini unataka kunieleza Victor? Akauliza Mathew


“Kaka utanisamehe nilikudanganya.Sikukueleza ukweli pale awali kuhusiana na hapa nyumbani” akasema Victor


“Kuna kitu gani kinaendelea hapa nyumbani? Nieleze kweli tafadhali” Akauliza Mathew na Victor akamueleza kila kitu kuhusiana na Gosu


Gosu,Mathew akahisi miguu inamtetemeka.


“Victor hilo unalonieleza ni jambo la kweli? akauliza Mathew


“Ni jambo la kweli kabisa bosi”


“Gosu Gosu amefungwa maisha gerezani? Akauliza Mathew na kugonga meza kwa hasira akashika kichwa


“Nilihisi kuna nguvu kubwa inanivuta nirejee nymbani kumbe ndugu yangu amekumbwa na masahibu haya makubwa.Yaani Gosu


Gosu maisha yake yaishie gerezani? Akawaza Mathew


“Natakiwa niende Arusha haraka sana.Siwezi kulala Dar es salaam wakati ndugu yangu yuko gerezani.Nataka nikafahamu kilichotokea.Nitapambana kufa na kupona kwa ajili ya Gosu Gosu lakini kwanza natakiwa kusikia kutoka kwake kile kilichotokea.Nataka nimtazame machoni akiri kama kweli alifanya kosa hilo la mauaji.Kama kweli alimuua huyo mwanamke kama inavyodaiwa nitahuzunika


sana kwani sintakuwa na namna ya kuweza kumsaidia kwani lazima sheria za nchi zifuatwe, lakini endapo hatakuwa ametenda kosa hilo ninaapa kufanya kila linalowezekana kuhakikisha Gosu Gosu anatoka gerezani ! akawaza Mathew na kuinamisha kichwa


“Furaha yote ya kurejea nyumbani imetoweka.Sikutegemea ningekutana na jambo ambalo lingeniumiza kama hili.Natakiwa nianze safari ya kuelekea Arusha


haraka.Nitasafiri usiku kucha na hadi kufika asubuhi nitakuwa Arusha.Nataka kitu cha kwanza kesho asubuhi iwe ni kuonana na Gosu Gosu” akawaza Mathew na kumtazama Victor akamtaka akafungue gereji ya magari akachagua gari ambalo angelitumia kwa safari ya Arusha kisha akaenda chumbani kwake akapakia nguo na vitu muhimu ambavyo angevihitaji akamuaga Victor akaondoka.


“Ee Mungu naomba uniongoze katika safari hii


niweze kufika salama Arusha.Nahitaji kuufahamu ukweli kuhusu Gosu Gosu kama kweli aliua mtu” akawaza Mathew akiwa katika kituo cha mafuta akijaza mafuta tayari kwa safari ya kuelekea Arusha


ARUSHA


Ilimlazimu Mathew kupumzika ndani ya gari baada ya kufika mjini Moshi usiku.Saa kumi na mbili za asubuhi akaanza safari ya


kuelekea jijini Arusha na kabla ya kufika saa moja za asubuhi tayari alikuwa jijini Arusha.Akatafuta hoteli nzuri na kupata chumba


“Ahsante Mungu kwa kunifikisha salama Arusha” akashukuru Mathew kisha akaingia bafuni kuoga halafu akapiga simu akaagiza apelekewe supu.Baada ya kupata kifungua kinywa akarejesha chumba na safari ya kuelekea katika gereza la Kimondo ikaanza.


Mathew aliwahi sana kufika pale gerezani na hivyo


kumlazimu asubiri kwani kwa muda aliofika wafungwa walikuwa bado katika majukumu yao ya asubuhi.


“Hili ni moja ya gereza lenye ulinzi mkali sana hapa Tanzania kuzidi hata lile la Uwangwa.Hapa wanaletwa watu waliohukumiwa kunyongwa na wale wa vifungo virefu kuanzia miaka thelathini.Inaniumiza sana kwa Gosu Gosu kujikuta sehemu kama hii.Natamani sana kuonana naye haraka haraka naona kama uvumilivu


unataka kunishinda” akawaza Mathew


Saa nne na nusu akachukuliwa na kupelekwa sehemu ambako angeweza kuonana na mfungwa aliyekwenda kumtembelea.Ulikuwa ni ukumbi maalum uliokuwa na meza kadhaa pamoja na viti.Ukumbi ulikuwa mtupu hakukuwa na watu waliotembelea wafungwa zaidi ya Mathew.Baada ya dakika kumi na tano Gosu Gosu akaingizwa katika ukumbi ule akiwa ameongozana na askari


magereza wawili huku mmoja wao akiwa na bunduki.


“Mathew ?!! akasema Gosu Gosu kwa mshangao mkubwa.Hakuamini kile alichokuwa anakiona mbele yake.Mathew alipomuona Gosu Gosu akasimama.Mathew akapewa taratibu kwamba haruhusiwi kugusana na mfungwa au kumpatia kitu chochote.Askari wale magereza wakasogea pembeni na kuwaacha akina Mathew wazungumze


“Sasa naamini kuna Mungu ! akasema Gosu Gosu na Mathew akatabasamu


“Kweli kuna Mungu na ukimuomba anajibu maombi ! akasema Gosu Gosu ambaye machozi ya furaha yalionekana katika macho yake.


“Gosu Gosu ! akasema Mathew


“Mathew kuna wakati sikuwa nikiamini uwepo wa Mungu lakini sasa ninaamini kweli kuna Mungu.Kwa wiki yote hii nimekuwa nikifanya maombi kumuomba Mungu kokote kule uliko kama uko hai


akurejeshe nyumbani na siamini kama kweli leo hii umefika hapa” akasema Gosu Gosu


“Stop crying Gosu Gosu.Soldiers don’t cry ! akasema Mathew


“Sioni maneno ya kumwambia Mungu ahsante kwa hili alilonitendea.Mathew dah ! akasema Gosu Gosu


“Pole sana Gosu Gosu kwa yote yaliyotokea” akasema Mathew


“Ahsante Mathew.Hadi umefika hapa naamini tayari umekwisha fahamishwa


kilichonitokea.Ndugu yako maisha yangu yameharibika na ninaozea mahala hapa.Maisha yangu yote yataishia hapa” akasema Gosu Gosu


“Gosu Gosu nataka kufahamu kilichotokea.Nieleze ukweli wote bila kunificha hata nukta moja” akasema Mathew


“Mathew siwezi kukuficha kitu chochote nitakueleza kila kitu kwani wewe ndiye mkombozi wangu” akasema Gosu Gosu na kuanza kumuelezea Mathew kisa chote tangu alivyokutana na Lidya


wakaanzisha mahusiano hadi kifo cha Lidya kilivyotokea.


“Hivyo ndivyo ilivyokuwa Mathew.Sikumuua Lidya.Ni mwanamke niliyempenda sana na tayari tulikuwa na mipango mingi ya kuhusu maisha yetu.Kwa ufupi tayari nilikwisha fanya maamuzi ya kumuoa Lidya.Naomba uniamini Mathew sikuua.Kama ningemuua ningekwambia bila kukuficha” akasema Gosu Gosu


“Nina kuamini Gosu Gosu.Swali linaloibuka ni nani alifanya mauaji hayo na kwa


nini? Unaonekana ni mpango ulioandaliwa kitaalamu mno na lazima ipo sababu kubwa ya kufanya hivyo.Umejaribu kutafakari kwa kina kwa nini mauaji yaleyakatokea na kwa nini jambo hili likakuangukia wewe na si mtu mwingine?


Akauliza Mathew “Nimetafakari sana.Kila


ninapokaa ninatafakari kwa kina kutafuta kwa nini jambo hili limetokea lakini bado sijapata jibu ila kuna mambo Fulani ambayo yanaweza yakatusaidia katika jambo hili.Baada ya kuja gerezani


nilianza kulitafakari jambo hili kwa kina.Nilikuwa navuta picha ya tukio lile na kujaribu kulichambua na kuna kitu nilikigundua ambacho sikuwa nimekigundua hapo kabla kwani nilikuwa nimechanganyikiwa” akasema Gosu Gosu na kunyamaza kidogo akamtazama Mathew aliyekuwa makini akimsikiliza


“Baada ya kuivuta kwa makini picha ya tukio lile nimekuja kugundua kwamba kompyuta ya Lidya ambayo alikuwa nayo kitandani wakati ninatoka kwenda jikoni


haikuwepo mle chumbani.Si kompyuta tu bali hata simu yake nazo haikuwepo mle ndani.Imenichukua muda kuligundua hili jambo”


“Una hakika Gosu Gosu?


Akauliza Mathew


“Ndiyo nina uhakika.Kama nilivyokwambia wakati tukio lile limetokea nilikuwa kama nimechanganyikiwa sikugundua lolote lakini baada ya kutulia na kuanza kurejesha kumbu kumbu za tukio lile ndipo nikagundua hilo jambo” akasema Gosu Gosu na Mathew akavuta pumzi ndefu


ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog