Search This Blog

Sunday 20 November 2022

URITHI WENYE UMAUTI - 5

 





    Simulizi : Urithi Wenye Umauti

    Sehemu Ya Tano (5)



    Sofia hakuwa na uwezo wa kufurukuta hata kiduchu, maana nilikuwa nimemfunga sawa sawa.Mitiririko ya jasho ikawa ikimtoka mwilini baada ya kuiona ile bastola niliyokuwa nimekamata mkononi.Mawazo mengi yalikuwa yakinipitia kichwani ya jinsi na ambavyo ningewapa adhabu wale watu wawili.Nikiwa katikati ya mawazo Yale,mlango ukagongwa na mtu kutoka nje pia akijaribu kuusukuma ndani ila akashindwa maana ulikuwa umekomelewa."Said harakisha tunahitajika na bosi!"Yule mtu wa nje alipaza sauti kumwambia mwenzake tuliyempata kwenye penzi zito na mpenzi wangu Sofia.Kimya kikafuata ila kwa kifupi kabla ya yule mtu kuongea tena.



    "Muda umekwenda Said,mbona hutoki au yule hawara amekutendea nini?"Yule mtu akasema.Niliusogea mlango kisha nikazungusha kitasa polepole,ukafunguka.Mwanamume mwenye urefu wa makamo akajitoma ndani muda huo nikiwa nimejibanza kando ya mlango.Alipofika ndani akamaka baada ya kumwona mwenzake amefungwa na Sofia.Nikauona mkono wake wa kulia ukifikia kiunoni nami sikuwa zumbukuku,nikang'amua njama ile mapema.Njama ya kuchomoa bastola."Usidhubutu!"Nikatoa amri kali iliyomshtua na kulazimika kugeuka,akawa akiangaliana na domo la bastola.Mshangao uliompata haukuwa wa kikawaida ila akawa akijikaza asiuonyeshe kwa vitendo."Iweke bastola chini pole pole la sivyo ninaufumua ubongo wako!"Nikamwamrisha kwa ukali.Lisilo budi hubidi,aliiweka bastola chini Kisha nikamwamuru asonge nyuma hatua nne,nami nikaitwaa ile bastola na kuiondoa usalama.Nikamnyoshea ile niliyokuwa nayo awali na kuvuta triga ikatoa mlio wa vyuma viwili vikigongana-kiashiria kuwa sikuwa nimebakiza risasi yoyote.



    Yule mtu kweli akaudhika,akiniangalia kwa macho yenye ghadhabu huku akijaribu kusaili jinsi angejiondoa mtegoni.Niliisundika bastola yangu kiunoni kisha nikaichukua ile ya yule mtu na nikampiga risasi moja mkononi.Sauti mbovu ya mfyatuko kutokana na kukosa kuwa na kiwambo cha kuzuia sauti ikasikika.Nikamwongezea nyingine iliyokifumua kichwa chake vibaya.Ubongo ukamwagika na kujipaka ukutani.Hali ya taharuki ikazuka mle ndani.Abdi akausogea mlango na kuchungulia Kisha akaniita kwa sauti."Roy,king'ora cha polisi!!".Nilimtazama Said kisha nikaamua kutomwacha bure.Nilimpiga risasi mbili kifuani,nikarukia mlango ila nikateleza na nilipokuwa niking'ang'ana kusimama,kidole changu kikavuta 'triger' risasi ikamcharaza Sofia begani upande wa kulia.Yowe Kali likamtoka.



    Niliungana naye Abdi tukatoka mle ndani na kuwafuata wale wanafunzi waliokuwa wikiparamiana ovyo ovyo.Waliokuwa nusu uchi hawakujali soni ila muda huo ulikuwa wa kuokoa maisha.Tulipishana na polisi wa kitengo cha ugaidi wakiingia kwa namna ya kupendeza.Nilikuwa nimeificha bastola niliyomnyang'anya yule mshirika wa Said kiunoni.Tulitokeza nje na kufululiza mpaka kwenye gari letu,tukajiweka vitini,Abdi akaiwasha nasi tukatokomea.Njiani tukapishana na magari aina ya lori,nne za wanajeshi wakielekea chuoni Romi.Tulifika jijini Sogomo kwake Abdi ikiwa imewadia saa nne usiku.Tuliingia ndani na kuoga Kisha Abdi akaanza kupika.Mimi nikaisogelea runinga ndogo mle ndani na kuiwasha.Nilitazama kwa muda kisha habari zikaanza kutangazwa.Butwaa iliyo



    nipata baada ya kuiona tukio ambalo tulilifanya chuoni Romi haikuwa ya kumithilika."Natumai u mzima mpenzi mtazamaji.Moja kwa moja tunaanza habari za leo rasmi ya mwanzo ikiwa tukio lililotokea chuoni Romi,moja ya chuo ambacho kinaaminika na kukubalika kama sio kuheshimika katika ukanda huu wa Afrika mashariki.Hii leo kumetokea tukio la kigaidi ambalo limetekelezwa na vijana wawili barobaro mmoja akijulikana kwa jina moja la Roy.Tukio hili lilitokea mida ya saa nane mchana wakati wanafunzi wengi walikuwa wamekwenda katika masomo ya mchana.Licha ya hayo kulikuweko na miili miwili ya wanaume kati ya miaka ishirini hadi thelathini.Hata hivyo msichana mmoja pia alipatikana akiwa na risasi moja begani muda huo akiwa amezirai.Mkuu wa idara ya usalama,Jenerali Yusuf Yudy amesema tukio hili linachunguzwa kwa undani."Mtangazaji akamaliza."Roy mambo yanakuwa magumu."Abdi akaniambia."Nikidhani yanibidi mimi mwenyewe nijitwike haya.Pole kwa kukuingiza katika hatari hii Abdi."Nikamweleza."Hamna shida Roy,usiwe na wasiwasi,mimi na wewe ni kama ndugu sasa.Mbona nikuachie msiba huu peke yako?"Abdi akaniambia.Kweli maneno yake yaliniliwaza kwa asilimia kubwa.Kwisha maliza shughuli za upishi,tulijiandaa na kujibwaga kitandani.



    Tukiwa tumelala,mara Abdi akanigusa begani akiomba tusemezane kabla ya kulala."Vipi Abdi?"Nikamwuliza."Roy,nimetafakari kuhusu hali iliyoko kwa Sasa.Kweli si hali nzuri ukijumlisha na hatari inayotukabili siku baada ya siku.Huwezi jua haya yote yatakwisha lini na vipi.Kulingana nami,naona Ni vyema ikiwa nasi tusake silaha za moto"Abdi alisema.Ukimya ukashika hatamu,takribani dakika tano kabla yangu kumjibu."Ni wazo zuri Abdi ila kuna ugumu fulani"."Ugumu upi?"Akauliza."Tutapata wapi zana hizi za moto?Pili,hatutakuwa tumewavuta karibu wanausalama na wanaintelijensia wa nchi hii?"."Hakuna ugumu wa yote hayo.Nina rafiki yangu humu mjini ambaye anakodi silaha halali ila si halali kwa asilimia fulani.Pia kuhusu kuziweka usiwe na wasiwasi.Tutatoboa sakafu ya chumba hiki kisha tunaunda kikabati cha saruji.Humo ndimo tutaziweka"Abdi akaelezea.Nikawa nimependezwa na mawazo yake.Tulijadili hili na lile muda mfupi tu,kisha tukalala.

    Alfajiri,tukaamka kujiandaa kuanza siku yetu.Nilipika chai tukanywa na silesi za mkate kisha Abdi akaanza kunipa maelezo ya jinsi na ambavyo tungempata yule rafiki yake,muuza silaha."Ila pesa ndiyo tatizo Roy.Mimi nimeishiwa kabisa,nimebakiza tu hela ya chakula"Abdi akasema."Usijali,ninazo za kutosha"nikamwahidi.





    'Jerusalem',ndilo jina lililokuwa limeandikwa mlangoni.Jumba lenyewe halikuwa limekamilika kujengwa.Vyumba kadhaa vilikuwa bado na vumbi na kokoto sakafuni.Mwenyeji wetu,kijana wa umri wa makamo ila aliyejengeka kimwili,alikuwa akitupitiliza hapa na pale mpaka ramani ya mle ndani ikanipotea akilini.Muda mchache,tukatokelezea kwenye chumba kilichokuwa kimepambwa kwelikweli.Kochi za mbonyeo,za kuvutia zilikuwa zimezunguka mle ndani.Tuliketi kisha Abdi akaanzisha mazungumzo moja kwa moja."Ni siku nyingi sana Yolanda tangu tuwe pamoja"Abdi akamsemesha yule kijana aliyemwita Yolanda."Kweli sahibu wangu,ila si tumekutana leo?"Yolanda akasema huku akitabasamu.Mazungumzo machache ya kirafiki yakachukua hatamu baada ya utambuzi kisha Abdi akamsimulia Yolanda masahibu yetu.Alimwelezea yote kuhusu kuuawa kwa wazazi wangu mpaka na matukio yaliyofuata baadaye."Pole sana Roy,kweli yote ambayo umeyapitia ni Rabuka tu ayajua"Yolanda alinipa pole huku akinipapasa mgongoni.



    Machozi yakawa yakinitiririka huku rundo fulani la uchungu likinipanda kooni.Abdi na Yolanda wakawa wakinituliza.Yolanda akasogea kwenye friji na kuchukua soda tatu aina ya Fanta,akavifungua na kutukaribisha."Hebu tuwe na kinywaji kabla ya kuendelea maana hali iliyopo si ya kupendeza na salama kwa rafiki Roy Sikazwe."Yolanda akasema.Kadri muda ulivyokuwa ukisonga ndivyo hasira ikaanza kunitoka,nikarudi katika hali ya kawaida."Sasa vipi kuhusu mihela ndugu zangu?"Yolanda akatuuliza."Hamna shida Bratha maana tumekuja tayari tayari"Abdi akamwambia."Ok,tuingie ghalani"Yolanda akasema.Nikasimama tayari kwenda kuzikagua zile silaha ila Yolanda akacheka pamoja na Abdi."Tulia Roy,twaenda sote tena kwa njia ya ajabu"Abdi akasema.Kwisha sema hivyo,nikamwona Yolanda akibonyeza kitufe fulani chini ya meza kikatoa mlio hafifu kama lile la mtu anapolikanyaga tawi lililokauka.Polepole sakafu ikawa inazama,kisha tukapokelewa na giza totoro ambalo halikudumu sana.



    Tukatua kwenye chumba fulani ardhini lenye upana mkubwa.Kilichonishangaza zaidi ni kuwa vile vyumba vyote vilikuwa na muundo sawa,pia samani ikiwa na mkao ulioshabihiana na mwingine.Sehemu kulikokuwa na friji kule juu ndiko kulikokuwa na friji huku chini.Lile sakafu ambalo lilituleta mle ndani likajirudisha kule juu baada yetu kuliondokea.Yolanda alisogea kochi moja refu Kisha akainama na kubonyeza kitufe fulani,nacho kikatoa sauti mfanano na ule wa kwanza.Kochi lile likajivuta nyuma na kuuwacha uwazi mkubwa tu kiasi ulioweza kuturuhusu kutumbukia ndani.Muda huo wote,hamna aliyemsemesha mwenzake.Tukafika ndani ya chumba chenye ukubwa kama wa ule wa juu.Tofauti ikiwa tu kuwa chumba tulichofikia kilikuwa kimejazwa silaha aina ainati ukutani.Kulikuwa na bunduki za walenga shabaha,zile ambazo niliweza kuziona kwenye runinga tu,nazo zikiwa mle ndani.Upande mmoja kulikuwa na bastola fupifupi,nami nikavutiwa na moja iliyolandana kimuundo na ile niliyokuwa nimewapokonya wale watu kwetu nyumbani."Chukua glovu hizi ndipo mzikague silaha hizi"Yolanda akatuambia huku akitukabithi glavu nne.Nilianza kuangalia moja kwa moja kila silaha iliyokuwa imenivutia."Ukuta ule unasilaha ndogo ndogo Kama vile visu vya kininja,sindano za kupuliza zenye sumu hivyo mjichunge navyo.Pia kuna grenedi za kurushwa na za kutega ardhini.Navyo msisahau mkachomoa pini ya usalama kwani zitalipuka."Yolanda alieleza akituonyesha ukuta wa nyuma kabisa.



    Baada ya ukaguzi wa hapa na pale,tukaanza kukusanya silaha moja moja mezani.Tukachukua bastola sita za aina tofauti,magazine mia moja zilizojaa risasi,bunduki nne za kijeshi,vilipuzi aina ya grenedi za kutupa na kutega na zile silaha ndogo zenye sumu.Kwisha maliza kuchagua,tukaanza kuvipaki kwenye begi tulilokuja nalo.Baadaye safari ya kurudi kule juu ikaanza.Tulipofika kwenye chumba cha kwanza,tukaketi tena kochini kujadiliana."Pesa zangu nitapata vipi?"Yolanda akatuuliza."Nakutumia hivi sasa kwenye simu yako"Nikamwambia."Sawa ila sifikiri ni njia nzuri maana hivi sasa wewe watafutwa na wale watu wasiojulikana.Ningeomba ile kadi yako ya mawasiliano niifutie mtandao wa 'tracking'"Yolanda akasema.Nikampatia ile kadi,naye akaipachika kando ya tarakilishi iliyokuwa kando yake,kisha akabonyeza vitufe kadha wa kadha na kuitoa ile kadi."Sasa nimeiwekea usalama na kuitolea ile ya awali.Upo huru kuitumia sasa."Yolanda alisema.Akanipa ile kadi,nikaipachika kwenye simu yake Abdi na kufanya malipo ya silaha zile.Nilibaki na kiwango kikubwa cha pesa kwenye akaunti yangu ya benki ya rununu.Tulimuaga Yolanda kisha tukaondoka huku akitusindikiza."Nawatakia kila la heri ila msisite kunijulisha iwapo mwahitaji msaada wowote"akatuambia."Ndio Bratha.Tukishindwa Lazima tukujulishe maana licha yetu kuwa wawili,bado methali isemayo;kidole kimoja hakimwui chawa,inakubalika"Abdi akamwambia Yolanda.



    Tulirudi kwake Abdi ikiwa imetimu saa nne usiku maana tulichukua muda mrefu kwake Yolanda,karibia siku nzima.Saa saba usiku ikatupata mezani,kwa harakati za kupanga namna ya kuanza vita vile."Ni vizuri tukianza uchunguzi nyumbani kwenu"Abdi akasema."Mmmh,vyema sana ila tutapita vipi mpaka ndani maana wale watu ninao uhakika watakuwa wameniwekea mtego"nikamweleza Abdi."Ndio maana tulitafuta silaha.Licha ya hayo,operesheni yote itafanywa usiku tukianza kesho.Kando na hayo,tutatumia majina bandia,wewe nitakuita Ahmed Musa nami utaniita Janito Kimbili"."Kwa nini tuitane majina bandia?"Nikamwuliza."Ili kuepuka uwezekano wetu kujulikana"Abdi alisema."Nimekumbuka kitu Abdi linaloniletea wasiwasi"."Lipi hilo?"."Iwapo Sofia atahojiwa na polisi na kunitaja itakuwaje?"









    MWISHO WA SEASON 1

    ENDELEA KUFUATILIA SEASON 2

URITHI WENYE UMAUTI - 4

 





    Simulizi : Urithi Wenye Umauti

    Sehemu Ya Nne (4)



    Jiwe moja ikanipiga kando ya sikio na kunisababishia maumivu yasiyomithilika.Hii ikanisababisha kuinama na kuruhusu mawe na vifaa vingine butu vilivyokuwa vinarushwa kwangu kukata hewa.Kuona vile nikachomoa bastola yangu kiunoni na kitendo kile kikawaogofya wale vijana wakaanza kusogea mbali kama mbwa koko.Sikutaka kuendelea kuwepo pale maana nilipoangalia nilipotoka nikawaona watu watatu,wawili wa kiume na mmoja wa kike wakija upande niliokuwa nikikabiliana na wale ombaomba.Nikajipenyeza kati ya vibanda vile na kuanza kutimua mbio za uhakika huku nikawa naviruka vidimbwi vya majitaka kimchezomchezo.Tayari mwili wangu ulikuwa umezoea sarakasi zile ngumu.Nilipofika eneo kulikokuwa kumejaa taka na mitungi mibovu ya plastiki,nilijificha pale na kutazama kule nilikotoka.Umbali ambao nilikuwa nimetoka ulikuwa mrefu sana.Nikawaona wale watu wakija upande ule lakini kwa taabu sana kwa kuwa walikuwa wakizama hapa na pale.Wote walikuwa na bastola mikononi ambazo sikujua miundo yake ni ipi maana zilikuwa ndefu kupita ile ambayo nilikuwa nayo.



    Niligeuza na kuendelea na safari yangu nikiwapuuzilia mbali wale watu.Akilini nikaanza kuhusisha tukio lile kwenye gereji nililotoka usiku ambako nilikumbana na mwanadada mmoja na mtu mwingine wa jinsia ya kiume wakiniwinda.Nao wale watu waliokuwa wakinifuata muda mfupi,kulikuwa na mwanadada ambaye alishahibiana na yule wa kule gereji akiitwa Ava ila wa kiume ndiye sikumkumbuka vyema.Wale watu kweli walikuwa na mtandao mkubwa sana.Safari yangu ikanifikisha kwenye eneo lenye biashara anuwai.Kulikuweko na akina mama wauza nyanya,mboga na matikiti huku wengine wakijihusisha na kuwakaanga samaki ambao walikuwa wakubwa.Upande mwingine wa barabara nikawaona wanaume wawili wakiwauza samaki wadogo wadogo waliokuwa wakijulikana kama 'omena'.Samaki hawa walikuwa wakitokea nchini Kenya Ziwa Victoria,Kisumu.



    Nikiwa nasomea shahada yangu ya uhandisi kule Uingereza,nilisikia tetesi kuwa kabila la Wajaluo ambao hujihusisha na biashara hii ya samaki 'omena' hawakuwauza kwa pesa.Tetesi zilidai kuwa wao(Wajaluo) hubadilisha samaki wale na ngono.Iliaminika kuwa wao walikuwa wakikubaliana na akina mama waliokuwa wakiwanunua samaki wale kubadilishana kwa njia ile.Dakika tano baadaye nikaona pahali ambako 'taxi' za kukodi zilikuwa zimepaki.Nilifululiza hadi pale ambapo kijana fulani mtanashati kati ya miaka thelathini akanipokea na kuniingiza garini."Dogo nikupeleke sehemu ipi maana naona umetokea CBD?"Yule kijana akaniuliza.Sikuwa na jibu la moja kwa moja hivyo nikamwamuru aendeshe tu nitamueleza.Haraka haraka nikawa nikifikiri pahali ambapo ningeelekea toka pale maana mji wa Sogomo ulikuwa haukaliki tena kwangu.Licha ya Hilo,nyumbani kwetu pia sikuwa na wakuishi naye maana watu niliokuwa nikiwategemea walikuwa wameangamizwa.Machozi yalianza kunibubujika mashavuni,sikujua hatima yangu ingekuwa vipi na wapi."Bratha mbona walia"ilikuwa sauti yake dereva wa 'taxi' lile iliyonishtua baada yake kunitazama."Hamna kaka.



    Nipo sawa tu"nilimjibu kwa kifupi."Mbona sijawahi mwona mtu aliyesawa akitiririkwa machozi?Kando na hayo unaonekana mwenye wasiwasi mwingi,kila muda mfupi watazama nyuma."Alisema dereva.Kwa kweli yule kijana alikuwa ameusoma mwenendo wangu vyema licha ya mimi na yeye kukutana kwa muda mfupi."Ni matatizo ya hapa na pale maishani"nikamjibu tena kwa kifupi."Matatizo gani yale?"Aliniuliza lakini nikabaki kimya.Maongezi Yale yalikuwa yameanza kuniudhi na kunichosha.Ukimya ukarudi tena mle ndani huku sauti iliyosikika pakee ikiwa ni mngurumo wa injini."Hujanieleza tunaelekea wapi"yule kijana akaniuliza."Mjini Kunaro"nikamjibu."Enhe!Kote kule muda huu?Huwezi kufika kule muda huu angalia hapa Ni saa kumi na nusu.Labda urudi mjini Sogomo uchukue chumba ulale usiku huu mpaka kesho"yule dereva akasema.Kweli alichokisema kilikuwa ukweli mtupu.Kufika mjini Kunaro ilikuwa ndoto ya mchana kutokana na muda kuwa umeenda sana."Sina hela zozote hata kidogo"nilidanganya.Dhamira yangu ilikuwa kufika kwa akina Sofia,mpenzi wangu."Na Mimi utanilipa nini maana tayari tumesafiri mbali sana toka mjini?"akaniuliza."Nilizobaki nazo"nikajibu."Ok turudi mjini.Nitakupa hifadhi kwangu usiku wa leo kisha kesho nitakuwahisha Kunaro"akasema kijana yule.Kiukweli nilifarijiwa na maneno yale toka kwa kijana yule.Moyoni nikajawa na furaha Kama kibogoyo aliyeota meno."Asante sana.Sijui nikushukuru vipi?"Nikamwambia."Huna haja maana wewe ni kama ndugu yangu licha yetu kukutana muda mfupi tu"akaniambia.Kwisha kukubaliana,aligeuza gari lile tukarudi mjini.Muda ulikuwa umesonga kwelikweli maana jua lilikuwa limeanza kuzama.Njiani tukawa tukipishana na magari mengi-si Lori,si mashangingi,yote yakiwa viashiria kuwa binadamu walikuwa wanaingia kwao,kupisha giza litawale.





    Tulichukua dakika ishirini hivi kufika alipokuwa akiishi yule kijana.Chumba alichokuwa akiishi kilikuwa cha kukodi.Kilikuwa na vyumba viwili,jikoni na chumba cha kulala,pia kulikuwa na kochi moja mle ndani lenye uwezo wa kuwabeba watu watatu tu."Karibu ndugu.Ila waitwa nani?"yule kijana akauliza.



    "Naitwa Roy,Roy Sikazwe"nikamjibu."Sasa Roy mimi ni Abdi Kanja.Naishi humu peke yangu hivyo kuwa huru"yule kijana,Abdi akasema.Nilimshukuru Abdi kisha nikajitupa kwenye lile kochi kwani uchovu ulikuwa mwingi.Abdi aliwasha jiko la mafuta ya taa na kuinjika sufuria alilokuwa ameweka mchele kisha akaanza kukatakata kipande kikubwa cha nyama ya ng'ombe."Je,taxi yako utaliweka wapi?"Nikamwuliza Abdi maana tulikuwa tumeliacha nje."Hukaa tu pale mpaka asubuhi.Hamna atakayeiharibu.Mbona kuna madereva wengi mtaa huu wanapaki yao mbele ya milango yao!"Abdi alinijibu.Chakula kilichukua muda mchache kuiva kisha Abdi akapakua kwenye sahani mbili huku akichanganya na ile nyama aliyokuwa amekaanga muda mfupi tu uliopita.Kwisha kula,tukaketi kochini huku tukipiga soga kuhusu mada ya hapa na pale.Kweli Abdi alikuwa muongeaji sana pia akiwa mjuzi wa mambo mengi.



    "Roy,uliniahidi kunielewesha masahibu yako.Huu ni muda mwafaka"Abdi akasema baada ya ukimya mrefu kati yetu kukatika.Sikuwa na budi,ikabidi nimsimulie yote yaliyonikuta.Nikaanza na historia yangu fupi ya masomo,kwa ujana wangu mpaka niliposafiri Uingereza kusomea uhandisi wa masuala ya kielectroniki.Kisha nikamsimulia jinsi niliporudi nyumbani kutokea jijini Kunaro kwa mpenzi wangu na kufika nyumbani kuwapata wazazi wangu wameuawa.Kweli nilipofika pale machozi yakanibubujika,Abdi akawa akinituliza kwa maneno yakuliwaza."Halafu ikawaje baada ya hapo?"Akauliza.Nikamweleza nilivyowatoroka wale watu kule nyumbani,Msituni Nyangumi hadi kwenye lile gereji nilikoponea chupuchupu kisha kule mapipani mpaka nilipoabiri taxi lake.Ilimchukua Abdi dakika tatu hivi kabla ya kuinua uso wake kunitazama.Alinionea huruma na kuniahidi kunisaidia katika kila hali."Pia Mimi nina simulizi inayoshabihiana na yako,ila nitakusimulia siku nyingine.Muda umesonga sana inatupasa tulale,kesho ni siku."Abdi akaniambia.Chumba chake Abdi kilikuwa kidogo ila iliyopangwa vizuri,kitanda kikubwa kikiipamba tokea katikati,nacho kikawa kimepunguza ukubwa mle ndani.Tukapanda juu na kujifunika blanketi kisha usingizi mzito ukanipitia.



    ****Niliamshwa na mtikiso wa Abdi akiniarifu kuwa muda ulikuwa umekwenda sana."Roy amka upate kiamsha kinywa.Tuna safari ndefu leo,angalia ni saa tatu kitambo"Abdi alisema.Niliamka na kuingia bafuni kisha nikakwenda kununua mswaki wa meno maana sikuwa nimesafisha meno yangu kwa muda na pia sikuwa nacho pale kwa Abdi.Kwisha maliza kupata kiamsha kinywa,nikajivika tena yale mavazi ya kikombati baada ya kutoa suruali fupi aliyokuwa amenipa Abdi.Kwa usiri nikaipachika bastola kiunoni na kuiteremsha shati,kuificha.Katika simulizi yangu sikuwa nimemweleza Abdi kuhusu ile bastola hivyo nikalazimika pia kutomweleza kuhusu yule mtu niliyemwua kule nyumbani.

    Muda mfupi baadaye,safari yetu kwenda mjini Kunaro ikang'oa nanga.fikra zangu zikaanza kuyarudia matukio yote ambayo yalikuwa yametokea tokea siku iliyopita.Maisha yangu yakawa yamegeuka shubiri.Ukimya ulikuwa umekita mle ndani, hamna aliyetamka chochote.Tulipishana na magari tofauti tofauti,mengine yakielekea mjini Sogomo tulikokuwa tukitokea huku mengine yakitupita.Kwa kweli hali ile ya yale magari ikawa ikinipa funzo fulani maishani.Kwenye maisha watu huwa tofauti Kama magari;kuna wale wanajaribu kufa na kupona kufika ulipokuwa huku wengine waking'ang'ania kukufikia ulipo hata kukupita ulipo.

    Tulifika Kunaro saa sita mchana.



    Biashara kadha wa kadha zilikuwa zikiendelea,kila binadamu akiwa kwenye hamsini zake.Wachuuzi wa karanga na soseji walikuwa wakijaribu kuwauzia abiria waliokuwa wameketi karibu na madirisha ya magari.Hatukupata usumbufu mwingi maana Abdi alikuwa akiendesha gari mbio huku tukisimama pahali palipokuwa na mikusanyiko ya watu.Tuliwasili katikati ya mji Kunaro saa sita na nusu mchana.Tulifululiza mpaka chuo kikuu cha Romi ambako alikuwa akisoma Sofia.Sikumjulisha ikiwa ningefika pale siku hiyo maana tangu nigundue kuwa wale watu walikuwa wakinifuata kwa kufuata mawimbi ya mawasiliano ya rununu yangu,nikachukua uamuzi wa kutoifungua kamwe.Tulipita kwenye lango kuu mpaka zilipokuwa hosteli za wasichana.Kwa vile nilikuwa nikijua chumba alichokuwa akiishi mpenzi wangu,tukafululiza naye Abdi mpaka kule.Hakukuwa na idadi kubwa ya wanafunzi mle ndani maana wengi wao walikuwa wamekwenda kusoma vipindi vya mchana.Sofia alikuwa anasomea udaktari mwaka wa tatu.Tulifikia mlango nambari sitini(60) alikokuwa akiishi Sofia.Ndani kulisikika mziki hafifu wa 'R n B',aina ya mziki ambao ulisadikika kuwa ulianzishwa na wazungu weusi mwaka wa 19''.Muziki uliendelea kuimba tukikaribia chumba hicho.Sofia alikuwa amenizoesha kuingia mule chumbani bila ya hata kupiga hodi.Kweli tulikuwa tumeelea kwenye penzi zito,tukawa kama upinde na mshale au tuseme ulimi na mate.Niliusukuma mlango na kuingia,Abdi akinifuata nyuma.***Picha niliyoikuta mle ndani,ikaufanya moyo wangu nusura unipasuke.Juu ya kitanda kulikuwa na miili miwili,zikiwa kwenye penzi zito.



    Sofia alikuwa amefunga macho huku akihema polepole ikawa nimepata jibu la mziki ule kuwekwa kwa sauti hafifu.Yule Mwanamume sikuweza kumtambua mara moja maana alikuwa amelala kifudifudi huku Sofia akiwa kingalingali.Abdi alisimama kando yangu,akiwa ameachama mdomo.Kweli hakukuwa na kiungo chochote mwilini mwangu ambacho kilikuwa radhi kusonga hata sentimita chache.Dakika chache baadaye,Abdi alisogea mpaka ilipokuwa redio ile Kisha akaizima kabisa.Kitendo kile kiliwashtua sana Sofia na yule mchepuko wake,mshangao niliouona usoni mwa Sofia ulikuwa wa kuogofya."Bebi mbona umeshtuka"yule mwanamume akamwuliza Sofia maana yeye hakuwa ameusoma mchezo.



    Lile likawa pigo la pili kwangu baada ya lile la kuuliwa kwa wazazi wangu.Hii leo mtu niliyekuwa namwamini alikuwa amenisaliti.Hasira ilikuwa ikinipanda,nikaangalia chumbani mle kifaa chochote nimwadhibu yule baradhuli sawasawa.Yule mwanamume alipogundua kilichotokea akaruka juu kama mtu aliyeingiwa na pepo.Sehemu yake ya siri ikawa ikinyong'onyea haraka ungedhani ni mmea kifaurongo."Baby,nini hiki?Nani hawa?"Yule mwanamume akamwuliza Sofia.Muda wote huo, Sofia alikuwa amejikunyata pale kitandani akiniangalia,mkono mmoja mdomoni mwingine akijaribu kujisitiri,machozi yakimtiririka.Abdi naye alikuwa amesimama palepale ilipokuwa redio ile,akitazama mchezo wote ulivyokuwa ukijianika mbele ya macho yake.



    "Sofia sababu ya haya yote ni nini?"Nikamwuliza Sofia ila akashindwa kunijibu.Muda mchache,yule mwanamume akashuka kitandani na kuvaa suruali yake ila kabla ya kuvaa shati lake,nikapata wazo.Nikakumbuka kuwa kiunoni nilikuwa nimebeba ile bastola ya wale watu.Haraka nikaichomoa.Kitendo kile kikawashangaza wote mle ndani.Abdi naye hakuamini kile alichokiona mbele yake,naye alikuwa katika hali ileile ya Sofia na mchepuko wake.Yule mwanamume alikuwa akitetemeka mwili wake wote."Lala kwenye sakafu mara moja"nikamwamuru,naye bila hiyana akatii.Akalala kifudifudi huku jasho likianza kumtiririka mgongoni.Nikamsongea Sofia pale kitandani,kisha kwa nguvu nikamnasa kibao,kilichombamiza ukutani huku ukemi ukimtoka.Nikamfuata na kumziba mdomo ila nilipogundua bado sauti ya kilio kilikuwa kikimtoka,nikachukua chupi yake na kuisokomeza mdomoni kisha nikamwinua mpaka kwenye kiti kilichokuwa mle ndani.Nikachanua shuka na kumfunga mikono na miguu.Dozi sawa ikafuata kwa yule mwanamume ambaye nilimfunga kwenye meza ndogo ya kusomea miguu yake ikawa ikielea.



    ITAENDELEA

URITHI WENYE UMAUTI - 3

 





    Simulizi : Urithi Wenye Umauti

    Sehemu Ya Tatu (3)



    "Hamjambo ndugu zangu"niliwasalimu,"safi tu bratha"mmoja wao,bonge la mtu akatangulia kunijibu baada yao kugeuka."Naomba kuonyeshwa nyumba za gesti"nikawauliza."Nyoosha upande ule mbele kidogo utakutana na hoteli Kisha fuata uchochoro wa kushoto.Utaona majumba ya kukodi"mtu yule akanielekeza.Baada ya kuwashukuru,nilifuata njia niliyoelekezwa na wale wahandisi wa magari.Mbele kidogo hatua Kama hamsini hivi nikakutana na bango lililokuwa na mchoro wa binti aliyekuwa nusu uchi ikiwa na maandishi ya kichina ambayo sikuielewa ng'o.Kuliwacha bango lile nyuma nikakutana na uwanja wenye upana sawa na ule wa mchezo wa miguu lakini ikiwa imejaa vyuma na magurudumu mabovu.



    Sehemu kadha wa kadha za magari zilikuwa zimekusanywa upande wa kulia zikingoja ukarabati au kubadilishwa skrepu.Kando na kelele zilizokuwa zikitokea nje ya uwanja ule,pahali pale palikuwa na ukimya wa ajabu.Mbele sikuona uchochoro wowote ambao ungenifikisha kwenye gesti za kulala jinsi lile bonge la mtu lilivyonielekeza.Ghafla kengele ya hatari ikagonga kichwani,uwezekano wa asilimia mia kuwa nilikuwa nimejiingiza kwenye domo la mamba-mtegoni!!Nilijipenyeza katikati ya vyuma vile Kisha nikaiona gari aina ya Toyota,muundo wa kizamani, iliyokuwa imeng'olewa gurudumu zote na kusimamishwa juu ya bati gumu kuzuia kutu kuharibu mwili wake.Niliichagua kwani ndiyo iliyokuwa karibu na nilipokuwa na kwa vile sikutaka kupoteza muda,nikaiendea.Nilipata ugumu wa kufungua milango yake kwani ilikuwa imeathirika na kutu lakini dakika chache tu nikawa nimejitoma ndani.Viti vya gari ile vilikuwa bado kwenye hali yake ya upya.Nilijirusha upande wa nyuma na kujilaza kwenye viti.Mwili wangu ukawa umepata burudisho ambayo nilikuwa nimeikosa kwa muda mrefu.Nilitazama saa yangu ya mkononi iliyoonyesha kuwa ni saa kumi usiku.Alfajiri ilikuwa karibu kuigubika nchi.





    Kivuli kutokana na kiwiliwili cha mtu ndiyo ilinishtua kutoka kwa starehe zangu.Nilichungulia dirishani kwa umakini bila kusababisha kelele yoyote mle ndani.Watu wawili,mmoja wa kiume na wa kike,walikuwa wamesimama karibu na gari lile nililokuwamo.Mwanamke alikuwa na mkoba mweusi ulioshabihiana na wangu Kisha mwanamume yule akawa ameikamata bunduki kubwa ya AK-47 mkononi kwa ukakamavu."Akina Jonah wamesema amekuja huku.Mbona hatumwoni?"Mwanamume yule alisema kwa sauti ndogo lakini niliyoisikia vizuri."Yawezekana ametorokea upande ule,kuliko na lori bovu lile"mwanamke yule akamjibu mtu yule.Ukapita muda mfupi kabla ya wawili wale kuzungumza tena kisha yule wa kike akasema,"mbona usimwulize mkuu 'atrack' simu yake Kisha atupe ramani ya aliko huyu kijana?



    "Mara moja nikajua kuwa wale watu walikuwa wakinifuata kwa kutumia GPS ya simu yangu.Haraka sana nikachomoa simu yangu na kutoa betri Kisha nikaitoa pia kadi ya mawasiliano na kuvihifadhi kwenye mifuko midogo iliyokuwa kando ya begi lile.Wale watu wawili walikuwa wamesogea umbali wa mita tatu hivi Kisha yule wa kiume akawa akibonyeza rununu Kisha akaiweka kwenye sikio."Hatujampata kwa sababu amepotelea sijui wapi…ndio…tupo kwenye gereji hivi sasa…hapana…tusimwue?Sawa Sawa"yule mwanamume akawa akizungumza na mtu mwingine upande wa pili ambaye sikuwa namjuwa.Ilikuwa ni Kama anapewa amri kuhusiana na mimi."Wanasemaje Ethan?"yule mwanamke akamwuliza yule wa kiume ambaye nikamjua, Ethan."Mkuu anasema wamepoteza mawimbi ya simu yake hivyo tuendelee na msako kote mjini hata kwenye majumba ya kulala ila akipatikana tusimwue."Ethan akamjibu."Tusimwue!!Hukumbuki Jana akina Liam wamepoteza mmoja wao kutokana na huyu bwege?"yule mwanamke akamaka."Nani aliuawa kwenye kundi hilo?Mbona sijapata taarifa yoyote?



    "Ethan akauliza,"akina Liam walikuwa wamerudi kwa yule bilionea kutafuta ufunguo wa lile kasha kisha wakampata mwanawe,mkuu anashuku alikabidhiwa ufunguo ule na babake kwa siri.Katika harakati za kuipekua jumba lile na pia kumsaka yule kijana,mmoja wao akawa amemkaribia lakini akaambulia kusafirishwa kuzimu kwani alipigwa kininja"yule mwanadada akamjibu Ethan kwa maelezo marefu.Kwa kweli moyo wangu uligubikwa na furaha kwa kugundua kuwa hata wale watu walikuwa wananiogopa kufikia hatua hiyo."Lakini Ava yabidi ugundue kuwa bosi na huyu kijana ni wa damu moja hivyo hatutakikani kumwua.Ni sisi tutimize kazi,tulipwe na turudi nchini kwetu."Ethan alimwambia yule mwanadada ambaye pia nikamjua alikuwa anaitwa Ava.



    Maneno ya Ava yakawa yameniacha njia panda.Ni nani yule ambaye tulikuwa na unasaba alikuwa akinisaka?Wale watu walichukua muda mfupi tu pale kisha wakaondoka huku nikikosa kusikia mazungumzo yao vyema kwani mwendo wao haukuwa wa polepole.Tayari kutokana na maongezi ya wale watu wawili; Ethan na Ava,vita rasmi kati yangu na mkuu wao ambaye sikuwa nikimjua ikawa imetangazwa rasmi.Simu yangu ya mkononi ambayo ilikuwa ikitumika kunifuatilia nikawa nimeizima hivyo kuwapoteza.Kitambo miale hafifu ya jua ilianza kujipenyeza kupitia kwenye vioo vya gari lile.Kutoka mle ndani nikapata fursa ya kusaili mazingira pahali pale.Ulikuwa uwanja mkubwa uliokuwa umezungushiwa ukuta wa mabati.Upande wa juu kulikuwa na lori moja bovu lililokuwa limetelekezwa la kubebea mchanga lakini lenye muundo wa kisasa.Kwa muonekano wake ni kama lilikuwa limehusika katika ajali mbaya sana kwani mbondeko ubavuni ulidhihirisha hivyo.





    Sikupenda kuendelea kukaa mle ndani zaidi kwani kitambo niligundua kuwa wale wahandisi wa magari Yale walikuwa washirika wa kuniwinda au labda wakukodiwa kunipokonya uhai wangu.



    Upekuzi nilioufanya mle ndani haukufanikisha kupata chochote cha umuhimu kwani lilikuwa gari bovu tu.Kwa utaratibu,nikausukuma mlango wa lile gari na kujitoa huku begi nikilivaa mgongoni.Hali ya anga ilikuwa shwari kabisa,mwanga na joto kutoka kwa jua ikawa imeruhusiwa kuibusu dunia.Mwili wangu ulianza kurudiwa na uhai huku shati na suruali zikiendelea kukauka.Nilianza kutembea nikienda uelekeo wa nyuma ya uwanja wa gereji lile bila ya kusahau kusaili usalama wa pahali pale.Kufikia uzio ule wa mabati,nikauruka kwa kujivuta na mikono.Ulikuwa uzio imara sana tofauti na nilivyofikiri mwanzo.Nilifikia nyuma ya duka la nguo ambapo sikupata ugumu wa kuendelea mbele baada ya kupata uchochoro ulionifikisha upande wa mbele.Wazo lilinijia la kununua nguo pale kwani nguo zangu zilikuwa zimechakaa na kuchafuka kupita kiasi.Mwanadada mmoja mrembo akanipokea mpaka ndani ambapo nilianza kupekua hapa na pale nikitafuta suruali na shati ambazo zingenipendeza.Baada ya upekuzi wa hapa na pale,nilivutiwa na suruali moja yenye muundo wa kikombati na tisheti moja nyeusi.Suruali ile pia ilikuwa yenye rangi ya weusi ila iliyokolea.



    Nikaendelea mpaka upande kulikokuwa na viatu,nikachagua buti moja ngumu ya kijeshi.Kwisha maliza kununua mavazi Yale,nilipachika kadi yangu ya mawasiliano na kuiwasha rununu kisha haraka nikaingia sehemu ya Mpesa nilikodhamiria kulipia.Muda mfupi tu nikawa nimemaliza kumlipa yule mwanadada kisha nikaizima tena rununu ile na kuchomoa kadi ya mawasiliano na betri.Nikaondoka eneo lile baada ya kuulizia zilipokuwa vyumba vya kukodi.Nilifululiza mpaka sehemu niliyoelekezwa na binti yule,nikakodi chumba kimoja.Kwisha kuoga,nikavaa suruali na shati niliyokuwa nimenunua muda mfupi tu nyuma.Kwenye kioo nikadhibitisha kuwa nilikuwa tayari kukabiliana na misukosuko yoyote.Usingizi ukanipitia nikiwa pale kitandani huku nikiwa nimevaa viatu vile.





    Ubishi wa sauti ya juu kati ya watu ambao walikuwa upande wa mbele ndiyo iliyonigutusha."Sisi hatuwaruhusu wateja wengine kuingilia starehe za wenzao.Hivyo nambari ya chumba mnachokitaka hamtapewa"sauti ya mwanadada wa mapokezi ikasikika."Sisi Hatuna shida nawe ila yule mvulana aliyechukua chumba humu"sauti ya kiume ikasikika.Machale yakanicheza,wale watu walikuwa wamenifikia tena mle niliokuwa nimejificha.Walipokuwa wakiendelea kubishana,nilishuka kutoka kitandani na kuvaa begi langu baada ya kuchomoa bastola niliyowaibia wale watu nyumbani kwetu.Sikujua ilikuwa imebakia na risasi ngapi ila hilo halikunibughudhi,ilmuradi tu nilitaka itumike kuwaogofya wale watu.Kwa uangalifu na polepole nikakinyonga kitasa cha mlango na kutoka Kisha nikaurudisha polepole.Kando na mabishano kule mapokezi,wapangaji wengine walikuwa kimya,kila mmoja akijihusisha na ya kwake.



    Nilitembea kwa kunyata nikichukua uelekeo wa zilipokuwa vyoo.Nikakata kona upande wa kushoto, nikawa nikiangaliana na mlango wa chuma uliokuwa umefungwa na kwa uchunguzi wa haraka,nikagundua kuwa mlango ule ulikuwa umefungwa kwa muda mrefu kutokana na kutu iliyokuwa imeanza kuiharibu kufuli ile.Haraka nikauparamia mlango ule na kutokea sehemu zilikokuwa vyoo ambavyo navyo havikuwa vimetumika kwa muda mrefu mpaka misitu midogo midogo ikawa imeanza kuota kwenye kuta.



    Mipasuko ya hapa na pale kwenye kuta ikawa dhihirisho tosha kuwa vyoo vile vilikuwa vimetumiwa miezi kama si miaka ya nyuma sana.Nyuma ya vyoo vile kulikuwa na uzio wa mbao ambao ulikuwa na urefu usio wa kawaida mpaka sikuweza kuona nini kinaendelea upande ule.Nilitembea haraka mpaka kwenye uzio ule Kisha nikaanza kuuparamia kwa ustadi na umakini.Kabla ya kufika upande wa juu,nikasikia sauti mbovu ya bastola isiyo na kiwambo cha kuzuia sauti ikifuatiwa na ukemi wenye kuashiria maumivu.Sikutaka kupoteza muda pale hivyo nikamaliza kuupanda uzio ule na kurukia upande wa pili.Nikawa na uhakika kuwa wale watu walikuwa wamempa mwanadada yule wa mapokezi tiketi ya kwenda kuzimu.Eneo nililotua lilikuwa uwanja wa kutupa taka taka.



    Kulikuwa na chupa za pombe, karatasi zilizorushwa ovyo ovyo,nguo kuukuu,mipira ya kondomu zilizotumiwa kwenye mapenzi ya kununua.Almuradi eneo lile lilikuwa na kila aina ya uchafu.Niliambaa ambaa kwenye ukuta ule wa mbao huku nikitoka nyuma ya vyoo vile, nilikuwa nafuata uchochoro ambao ulielekea kwenye mabanda ya walalahoi.Nikawa nimeiacha eneo lile kwa mbali sana.Jua lilikuwa linachoma kwelikweli mpaka jasho ikawa ikinitiririka.Vibanda vile nilipovifikia,nikakutana na kundi la vijana wakibugia makombo ambayo sikujua vilikuwa mabaki ya vyakula gani.Waliponiona wakasimama huku wakianza kupiga kele kwa lugha ya sheng',ambayo sikuielewa katu.



    Mmoja wao akaanza kunikaribia kwa kasi ya ajabu huku akiwa na kipande cha chupa amekiinua mkononi nami bila kupoteza wasaa nikajitayarisha kwa vurugu lile.Muda wote ule wale wenzake walikuwa wakishangilia.Nikaona uwezekano wa kumdhibiti yule ombaomba ilikuwa ni kwa kumkita teke la nguvu tumboni.Aliposogea nilipokuwa,nikajipinda na kumchapa teke moja maridadi ikijulikana kana 'roundhorse kick'.Kutokana na ugumu wa viatu nilivyovivaa,mvulana yule akajishika pale teke lilikita Kisha akapiga ukemi.Wale wengine kuona hivyo wakaokota vifaa vyovyote vilivyokuwa vigumu ardhini na kuanza kunitupia.



    ITAENDELEA

URITHI WENYE UMAUTI - 2

 





    Simulizi : Urithi Wenye Umauti

    Sehemu Ya Pili (2)



    Mji uliokuwa umewameza vijana na wazee waliokuwa wapenda raha,si disko,si baa za kunywa pombe,si madanguro ambako mapenzi ya kiholela yalikuwa yakifanyikia.Almuradi chochote ambacho kilikuwa ni cha kuwafurahisha wapenzi wa anasa kilipatikana mjini Sogomo.Ari ya kutembea niufikie mji huo ikawa imeniingia,nikapata nguvu ya kutembea kufika kule.Mvua sasa ilikuwa imeongezeka, mitaro kando kando ya barabara ikaanza kupwa.Dakika hamsini baadaye nikawa niko hoi bin tiki kwani sikuwa mzoefu wa kutembea masafa yale marefu bila ya gari ya baba niliyokuwa nimezoea kuiendesha.



    Nikajibwaga chini kama mfuko wa viazi kwenye nyasi ndefu kando ya barabara.Nikiwa naendelea kupumzika pale,ghafla nikasikia gari likifungia breki mita takribani kumi toka nilipokuwa nimelala.Taa zote zilikuwa zimezimwa.Niliinuka polepole na nilipochungulia nikawaona watu wale wale niliokuwa nimewaacha nyumbani kwetu huku wakiwa na bunduki kubwa kubwa.Kufikia hapo sikutaka kupoteza muda nikingoja niuawe.Nilichomoka toka pale chini na kutokomea kwenye shamba la miwa lililokuwa karibu na barabara ile."Simama Roy!Hatuna nia ya kukudhuru"sauti ya kiume ilisikika tokea nyuma.Nilishangaa watu wale kuniita kwa jina.Maswali ambayo sikuwa na majibu yakanipitia akilini.Kwa nini wanifuate na silaha za Moto ikiwa hawana nia mbaya?Mbona baba na mama wageuzwe wafu bila sababu?Uzumbukuku haungeniingia niwaamini wale watu na kurudi au kusimama.Niliendelea kukimbia huku nikiziwacha shina kadhaa za miwa zimevunjika.Kelele ya matone ya mvua juu ya matawi ya miwa ikasababisha mimi kutojua walipokuwa watu wale.



    Nilipiga magoti mchangani na kuangalia nyuma nilikotoka vyema;hakukuwa na dalili ya mtu yeyote ila hili halikunifanya kupuuza hisia zangu kuwa eneo lile lilikuwa hatari kwangu.Muda mfupi nikasikia matawi ya miwa yakitoa sauti karibu tu na pahali nilipokuwa nimejificha.Kiwiliwili cha mtu kikajitokeza huku mtu yule akitazama kwa umakini,mkononi alikuwa amebeba sigara aliyokuwa akivuta kwa mikupuo,ila ikambidi kuiwasha mara kwa mara kwani maji ya mvua yaliizima.Sikuona silaha aliyokuwa amebeba mwanzo,ila mara moja moja nikaona chuma iking'aa sigara yake ilipokuwa ikitoa mwanga mdogo, uthibitisho kuwa alikuwa na silaha.Alinitafuta kwa kupigapiga matawi ya miwa kutumia bunduki ile ila akawa amenikosa.



    Muda mchache mtu yule akatokomea kwenye majani akifuata uelekeo wa tulipotokea baada tu ya maji kuizima sigara yake tena.Sikujua wale wengine walikuwa wametokomea wapi licha ya kuisikiliza redio niliyokuwa nimempokonya mmoja wao kule nyumbani.Akilini nikajua mchezo wangu umeshtukiwa.Kimya kimya nikaanza kutambaa ardhini nikielekea mbele na baada ya muda mfupi nikasikia sauti ya maji mengi Kama ya mto uliofurika mpaka kuvunja kingo zake.Nilijivuta matopeni nikielekea kulikokuwa kuna yale maji.Umbali wa takribani mita ishirini,nikayaona maji ya mto ule yaliyokuwa yakienda kwa kasi huku matawi ya miti yakiwamo.Nililisaili eneo lile na baada ya kuhakikisha usalama nikaketi kando ya mto ule ambao sikuwa najua jina lake kwa sababu yangu kuishi Uingereza na hata kusomea kule kabla ya kuitwa nyumbani na baba wiki chache tu zilizokuwa zimepita.Mara kadhaa nililetwa na baba nchini kuwatembelea nyanya na babu nyakati za likizo licha yangu kuzozana naye mara nyingi."Sasa ni kwa nini usije ujuane na wenzio?



    "Baba alipenda kuniuliza kila nilipoleta upinzani wa kurudi nchini"Mbona Mimi sioni shida kuishi huku baba?Nitawajua baadaye"nilikuwa nikimjibuu baba."Lazima uje Roy,hivi ukijipata umempachika mimba msichana wa ukoo wenu bila kujua kutokana na mahusiano yenu Yale ya kiholela utaficha wapi uso wako?"Baba angesema nami kwa kukosa be wala te ningekubali lakini shingo upande kurudi nchini Umalia.Nilikuwa najaribu kupata hewa safi na kupumzika.Sauti ya bastola ikiondolewa usalama ndiyo ilikanigutua kutoka kwa tafakuri yangu nzito,ikawa kupoteza muda pale kulimaanisha kupoteza uhai kiuzembe.Nilijitupa kwenye mto ule huku sauti hafifu ya risasi ikiibusu maji sentimita chache toka mguu wangu ulipokuwa kisha baadaye nikasikia sauti ya watu wakilumbana kwa muda mfupi tu maana maji yale yalikuwa na nguvu na yenye kelele nyingi.Yalinisukuma na kuniteremsha ila ujuzi wangu wa kupiga mbizi ukawa umeniokoa,nikaendelea kuelea huku nikijitahidi kuangalia ule upande niliotokea.Kwa taabu nikaweza kuwaona wanaume wale wakimulikamulika majini na kurunzi kubwa kubwa kwa jitihada za kunisaka kwani lazima walikuwa wakijipa moyo kuwa nilikuwa palepale



    Baadaye nikawapoteza kwenye macho yangu kutokana na kusukumwa na maji yale umbali mrefu sana.Nikamshukuru Mungu kwa kuniokoa toka domoni mwa simba.Maji Yale yalinipeleka mpaka pahali fulani nilipoanza kusikia sauti kubwa ya maji iliyotokana na muanguko wake kwenye mawe nami nikajua nimefikia (waterfall).Nilijua iwapo ningeendelea kubebwa na Yale maji,ningepasuliwa juu ya mawe chini ya waterfall ile.Kwa kutumia nguvu zangu za mwisho,nikapiga mbizi na kujivuta kutumia mizizi ya miti iliyokuwa imejitokeza kwenye kingo ya mto huo mpaka nikafaulu kutoka,licha ya kuwa nilikuwa nahema sana.Kufikia pale nilikuwa nimeloa chepechepe,yale mavi ambayo yalikuwa mwilini yakawa yameoshwa mbali nami nikawa nimeyabugia maji ya kutosha.Nilipofika ukingoni nilitulia kuvuta hewa baada ya patashika ya muda huo mrefu iliyokuwa imeniwacha hoi kwelikweli.



    Usaili wangu wa mazingira niliyokuwa ulinidhibitishia kuwa upande niliokuwa kulikuwa na msitu ambao sikujua ukubwa wake,ila nikakumbuka baba akiniambia uliitwa Msitu Nyangumi.Alinisimulia jinsi yeye na ndungu zake Mapipa na Sebastian walikuwa wakiwawinda ndege na wanyama wengine wadogo mle msituni.Kweli niliwaonea fahari maana baba alikuwa akinisimulia kwa namna ya kuvutia sana.Pale kijijini Kiwanika,baba alikuwa akiheshimika sana kutokana na utajiri wake bila kusahau misaada tofauti tofauti alizokuwa akiwapa wanakijiji bila kusahau genge la vibarua ambao walikuwa wameajiriwa kuchapa kazi shambani.Ndugu wa baba hawakuwa wakiishi Kijiji kile Bali walikaa mbali,kijijini Mapweke.



    Ami Sebastian hakuwa na mazoea ya kufika pale nyumbani ikilinganishwa naye ami Mapipa.Kando na hayo kulikuwa na mapenzi makubwa kati ya baba na ndugu zake.Upande mwingine wa mto ule kulikuwa na muendelezo wa shamba lile la miwa.Nilitoa mkoba wangu mgongoni nikafungua ndani na kuchomoa simu yangu ya mkononi iliyokuwa imetengenezwa mpaka haingeweza kuharibiwa na maji,kwa kimombo ikiitwa "waterproof".Niliifungua na kupunguza mwanga wake Kisha nikagundua ami Mapipa Yohana alikuwa amenipigia mara tano.



    Sikujua ikiwa alikuwa akinitafuta kuhusiana na kifo cha baba na mama au alitaka kuhakikisha usalama wangu.Kuachana na pale,niliingia kwenye mtandao wa WhatsApp,nikapata missed call nne za mpenzi wangu Sofia huku ikiambatana na jumbe chungu nzima alizokuwa amenitumia akinitafuta,jumbe ambazo sikuweza kuzisoma kutokana na mazingira na hali niliyokuwamo.Kengele ya tahadhari ikagonga kichwani mwangu baada ya kukumbuka missed call za ami ila sikujua ni kwa nini nilihisi vile kumhusu lakini singeweza kupuuza hisia zangu.Mbona mjomba na mpenzi wangu wananisaka namna hii?Niliirudisha simu ile mfukoni kisha nikaipachika mgongoni na kusimama.



    Mwendo wangu ulielekea upande wa msitu ule ambao sikuwa naujua kwa vyovyote.Ilikuwa ni afueni kuwakuta wanyama wakali kuwaliko wale watu waliokuwa wakinifuata,dhamira yao ikiwa ni kuniangamiza.Mvua iliendelea kunyesha hivyo kusababisha matope kuwa mengi ardhini, mwendo ukawa wa konokono.Baada ya kusonga umbali wa takribani mita hamsini hivi,nikageuka na kuona mwanga wa kurunzi uliokuwa na nguvu,mhusika akiwa anamulika pale nilipokuwa nimeketi hapo awali.Hisia zangu zikanitahadharisha kuwa eneo lile pia kulikuwa kumetangazwa vita kirasmi.Bastola ya wale watu niliyokuwa nayo sikujua ilikuwa imebaki na risasi ngapi nami sikutaka kubahatisha hivyo nikajaribu kuvuta chini kunakowekwa risasi.Juhudi zangu ziligonga mwamba kwani sikuwa na ujuzi wa kutumia silaha.Niligeuka na kuingia msituni nikiwa nakimbia.



    Mwili ulikuwa umekufa ganzi lakini singeiruhusu hali hii kunisimamisha.Niliendelea kuingia ndani kabisa huku nyuma nikiwa nafuatwa na wale watu unyo unyo.Giza totoro lilikuwa limetanda kotekote mpaka uwezekano wa kutazama sentimita chache tokea usoni ulikuwa mchache ila sikutaka kutumia mwanga wa rununu yangu maana ungekuwa chambo cha kuwavutia wale watu.Masaa mawili niliyatumia kuwahepa wale watu tu ila wahenga waliamba,mbio za sakafu huishia ukingoni,kwa mbali nikaona maji yaking'aa ardhini nikajua nimefikia barabara ya lami.Punde nikasikia sauti ya mngurumo wa Lori likija upande niliokuwa.Mwingereza alisema "opportunity avails only once' yaani bahati huja mara moja.Ilinipasa niitumie Lori lile kama njia ya kusafiri toka eneo lile.





    Mvua ilikuwa inanyesha kwa matone hafifu tulipokaribia mji wa Sogomo.Biashara kadha wa kadha zilikuwa zikifanyika huku wachuuzi wa vyakula aina tofauti tofauti wakiwauzia watu.Kelele zilikuwa nyingi pahali pale,nayo ikawa ni bahati upande wangu kwani licha ya kutua chini kwa kishindo,hamna aliyenitilia shaka au kuvutiwa nami.Labda walidhani nilikuwa omba omba wa mitaani.Niliyapita majumba ya disco yaliyokuwa yakipiga mziki kwa sauti ya juu.Wasichana waliovaa nusu uchi huku wakijiviringishia kwenye nguzo zilizokuwa zimetengenezwa katikati ya meza walikuwa kiburudisho kwa wahusika mle ndani.Kulikuweko na akina baba waliokula chumvi,rika la kuitwa babu na akina mama ambao waliteremsha vyupa zaidi ya viwili vya pombe kwenye matumbo yao.Almuradi burudani yoyote ilikuwa inapatikana humo.





    Mguso wa mtu kwenye bega la kulia ndiyo iliyonigutua toka kwenye mawazo yangu.Kugeuka nikakutana na tabasamu nyororo ya changundoa wakijulikana sana kwa jina la malaya kule Sogomo.Alikuwa amevalia sketi fupi na iliyokuwa imembana sana mpaka mchoro wa nguo yake ya ndani ikawa ikionekana."Naitwa Emma,Emma Mwagasaya.Ungependa tupitishe usiku huu nawe?"Aliniuliza "Sidhani"nilimjibu kwa mkato kwani sikutaka kuendelea na mazungumzo yale maana sikuwa na uhakika wa usalama eneo lile.Kwisha kumjibu,nikageuza na kujipenyeza katikati ya majumba mawili yaliyokuwa yamepakana.



    Uchochoro ule ukanifikisha mbele ya gereji la magari iliyokuwa na magari mabovu takribani ishirini kwa hesabu ya haraka.Wahandisi wanne walikuwa wakiikarabati shangingi moja aina ya Vitz nyeusi yenye nembo ya kikundi cha YDI ubavuni.YDI kilikuwa kikundi cha kuwainua vijana kiuchumi kwa kuwapa mikopo ya kuanzisha biashara ndogo ndogo humo nchini,kwa kirefu ikijulikana kama Youths Development Initiative.Mwili wangu ulikuwa umegubikwa na uchovu,nikaamua kuwaulizia wale wahandisi kulikokuwa na majumba ya kukodi ya kulala.





    ITAENDELEA

URITHI WENYE UMAUTI - 1

 





    IMEANDIKWA NA : POWEL CHEMOS



    *********************************************************************************



    Simulizi : Urithi Wenye Umauti

    Sehemu Ya Kwanza (1)



    Mvua kubwa iliyoambatana na upepo mkali iliendelea kunyesha hivyo kusababisha ardhi iwe yenye matope mazito.Niliendelea kukimbia huku nikichukua muda mfupi sana kupumzika bila ya kusahau kuangalia usalama wa eneo hilo.Giza nalo lilikuwa limetanda eneo lote mpaka nikashindwa kuisoma ramani niliyokuwa nimepewa na baba yangu,Yohana Sikazwe.Angalau kungekuweko na mwanga ningejua nilipokuwa naelekea.Nilijivuta kwa nguvu mpaka kwenye mti niliokisia kuwa wa mbuyu kutokana na umbo wa matawi yake.Kwa kweli nilikuwa nimeloa chapachapa,kaptura na shati zikawa zimenikwamilia mwilini.Niliuegemea mti huo huku nikitazama upande niliotoka.



    Nusu saa hivi,niliona mwanga kutoka chini ya kilima nilichokuwa nimeukwea muda mfupi tu nyuma.Dakika chache baadaye nikawaona watu wawili wakiungana na yule wa kwanza kutokea pande tofauti tofauti za msitu huo.Niliendelea kuwatazama,nikagundua kuwa walikuwa wakinifuata kutumia uelekeo wa alama za miguu yangu,nikang'amua kuwa uwepo wangu pale ungeniletea umauti.Niliikunja ramani yangu, niliyokuwa nimepata ugumu wa kuisoma,na kuiweka kwenye mkoba kisha kwa tahadhari ya hali ya juu,nikapenyeza kati ya msitu na kupotea.Nilipopotea kwenye upeo wa wakimbizaji wangu,nilitimua mbio za kikweli huku kila baada ya muda mfupi nikiangalia nyuma.Sikuwa najua ninakokwenda,mwisho wa mbio zangu sikung'amua ungekuwa wapi.Nilikuwa nimegeuka kuwa mkimbizi asiyekuwa na mbele Wala nyuma.Nilikuwa nikitembea kwa shida kutokana na kutokuwepo na mwanga wa aina yoyote,hata mbalamwezi au nyota angani.Hali hii ikafanya nikwaruzwe na vijiti na pia kugongana na mashina ya miti



    Anga lilikuwa limegubikwa na mawingu mazito yaliyosababisha mvua kubwa ikiambatana na radi.Mara anuwai niliweza kutazama kutumia mwanga uliosababishwa na radi ila nikapata ugumu wa kutumia kuisoma ramani niliyopewa na baba kwani mwanga ule ulidumu kwa sekunde chache tu.Mwendo wangu ulikuwa wa wastani hii ni baada ya kuwapoteza wale watu waliokuwa wakinifuata kutokea nyumbani kijijini Kiwanika tulikokuwa tunaishi.Taswira niliyoipata nyumbani kwetu jioni ile iliendelea kujirudia akilini.Kitendo cha baba na mama kuchinjwa Kama kuku kilinighadhabisha sana.Sikuwa mjuzi wa masuala ya kijasusi lakini kwa mtazamo wa jumba letu,niligundua kuwa lilikuwa limepekuliwa kwa ustadi na uangalifu wa hali ya juu.Niliingia kwenye chumba cha wazazi wangu kwa tahadhari nikitafuta chochote ambacho kingenipa mwanga wa unyama ule.Wakati wote huo,mtima ulikuwa ukinidunda mpaka nikawa nausikia kwa mbali bila ya kusahau mitiririko ya jasho usoni na mgongoni.Chumba hakikuwa kimeguswa,vitu vyote vilikuwa vimepangwa vizuri.Macho yangu yakang'amua uwepo wa karatasi ya kitabu iliyokuwa na maandishi ya kalamu dirishani.Nilisogea polepole Kisha nikaichukua na kuanza kuisoma.Ilikuwa barua fupi iliyosomeka hivi:"Mwanangu Roy,mimi na mamako hatuna muda mrefu wa kuishi ila twakutakia maisha mazuri hapo baadaye.Nataka kukupa urithi wa Mali yangu yote ila utabidi ujikaze kiume kwani tunaandamwa nawe utaandamwa.Usimwamini mtu yeyote.Chukua ufunguo kwenye kabati nimeificha Kisha uondoke.Baaada ya yote kupita,mtafute Padre Hiza Sibomane Marcus atakusaidia.



    **Wako akupendaye Yohana.Ilisomeka barua ile.Bila kupoteza muda,nilikimbilia jikoni nikafungua kabati ya vyombo na kweli baada ya upekuza,nikafaulu kupata ufunguo uliokuwa na umbo la kipekee,ukiwa umefichwa chini ya kikombe cha udongo.Ghafla,nikasikia sauti ya mkwaruzano wa ardhi na gurudumu la gari.Moyo ukaanza kunidunda,sikujua ni hatari ipi nilikuwa nikabiliane nalo.Nilichungulia dirishani na kwa usaidizi wa taa za nje,nikaiona gari aina ya Harrier yenye rangi nyeusi.Dakika chache baadaye milango ikafunguka kila upande kuwaruhusu wanaume wanne wenye miili iliyojengeka kimazoezi kushuka.Mwendo wao na jinsi walivyokuwa wakitazama ikanipa wasiwasi mkubwa.Mara moja wote wakachomoa bastola kutoka kwenye makoti yao na kuzikoki nami nikajua kuwa kazi imeanza.Niliondoka pale dirishani baada ya kugundua mmoja wa watu wale alikuwa ametazama pale kwa muda napo pakawa pamemvutia kwani alipakodolea macho sana.Singeweza kuwatambua moja kwa moja kwani walikuwa wamejivika miwani myeusi usoni.Nilitembea haraka haraka nikielekea pande za vyoo.



    Dhamira yangu ilikuwa kutorokea kule lakini kumbe mpango wangu ulikuwa umegonga mwamba.Kabla niufikie mlango huo,nikasikia mlio wa mtu akizungusha kitasa hivyo nikalazimika kujificha kwenye kona ya mlango.Polepole mlango ukafunguliwa kisha kiwiliwili cha mtu kikafuata.Alikuwa amekamata bastola mkononi huku domo lake likiwa limeelekezwa mbele."Ninaingilia upande wa vyoo,hakikisheni mnamtafuta na kuchukua ufunguo kwani bosi anahitaji.Harakisheni"mtu yule alisema akiwa ameegemeza kichwa upande wa kulia.Hapo nikajua kuwa walikuwa wanatumia redio za wanapolisi.Uwezekano wangu wa kutoka pale ulikuwa mdogo sana,nilihitaji kujitetea,lakini sikuwa na silaha yoyote ambayo ningetumia ila funguo na mkoba wangu.Kwa nyota ya jaha,nililiona spana alilokuwa akitumia baba kutengenezea gari lake wakati gurudumu lingekuwa na hitilafu.Nililiokota polepole bila kumshtua mtu yule kisha kwa nguvu zangu zote,nililinua juu na kumteremshia pigo lenye uhakika.Dhoruba lile likaipasua kichwa cha mtu yule nao mguno wake ukawa hafifu sana,akaanguka chini na kutulia kimya huku damu ikianza kuchuruzika kama bomba bovu la maji inayovuja.



    Nilichukua bastola yake na kijiredio cha kipolisi alichokuwa nacho.Niliisunda mfukoni na kuelekeza bastola ile mbele kama njia ya kujihakikishia usalama tosha.Hiyo ndiyo ikawa mara yangu ya kwanza kushika bastola.Nilinyata mpaka chooni nikachunguza nitakapotorokea,mara moja nikakumbuka mfuniko wa choo uliokuwa na mfereji kuelekea kwenye bwawa la kukusanya uchafu wa choo na maji machafu kutokea maliwato.Nje nilisikia sauti ya watu wale wakitembea kuja uelekeo wa vyoo.Haraka haraka niliinua kifuniko Kisha nikatanguliza mkoba wangu nami nikafuata.Harufu ya mle ndani ilikuwa ya kutapisha ila nilijikaza kiume,bastola nikiwa nimeikamata sawasawa mkononi.Mwendo wangu mle ndani ulikuwa wa haraka kwani kinyesi na mkojo vilisababisha utelezi mkubwa.Mavazi yangu yote yakawa yameloa kwa uchafu ule.Sikuwahi kufikiri ikiwa mimi,mwana wa bilionea mashuhuri,ningejipata katika hali hiyo.



    Safari ile ya dhiki ikaishia kwenye bwawa la kinyesi iliyonifikia kiunoni.Nilijikakamua nikaruka na kukipiga kifuniko cha kufunika bwawa lile kwa teke yenye nguvu,nikapata uwazi wa kutokea.Sikutaka kupoteza muda mwingi hivyo nilijivuta mpaka nje,nikapata kuvuta hewa safi iliyonirudishia uhai na uchangamfu.Nilichukua mkoba wangu na kuondoka pahali pale haraka.Baada ya kupiga hatua kadhaa tu mbele,nilisikia michakato ya miguu ikija upande ule.Haraka nikajibanza kwenye maua yaliyokuwa yameota pale bastola ikiwa tayari kutema cheche za moto.Muda mfupi tu baadaye,watu watatu wakatokezea wakiongea kwa sauti ya juu,dalili tosha kuwa nilikuwa natafutwa mzima au mfu.Mmoja wao aliusogea mfuniko wa bwawa lile na baada ya kuchunguza kwa umakini,akawaita wale wenzake.



    Niliwaona wakielekeza vidole vyao pale kisha mmoja akatoa kurunzi ndogo iliyofanana na kalamu kwa muonekano lakini yenye mwanga mkali sana.Alianza kuja uelekeo niliokuwa kwa kufuata matone ya kinyesi yaliyokuwa yakianguka toka mwilini mwangu,hapo nikajua kitumbua kimeingia mchanga.Nilijipa ujasiri na kujichomoza toka nyuma ya mti ule na kuiruhusu bastola kuachilia risasi ambazo sikujua idadi yazo kuwaelekea wale watu.Kitendo kilichotokea pale kiliniwacha mdomo wazi ,wanaume wale walijiviringisha hewani kwa sarakasi ya hali ya juu na kujitupa kwenye maua.Hakukutokea ukelele wowote kwani bastola ile ilikuwa imefungwa kiwambo cha kuzuia sauti,hivyo kukasikika sauti mfano wa kikohozi cha mzee mkongwe.Mvua ilikuwa imeanza kunyesha lakini kidogo sana.Mara moja moja kulisikika mlio wa radi na mwangaza uliofanya giza lipotee kwa muda mfupi.



    Watu wale hawakuwa wakionekana licha yangu kuchunguza kwa uangalifu eneo walikoangukia.Sikutaka kutumia risasi zingine maana ingekuwa kazi bure.Sauti fulani ndani yangu ilinitahadharisha-usalama wangu eneo lile ulikuwa wa kutilia shaka.Nilichukua begi langu mgongoni kisha bastola mkononi,nikatundika guu begani nikifuata uelekeo wa msitu Nyangumi.Punde tu niliporuka uzio wa nyumbani uliokuwa umetengenezwa kwa saruji na matofali,nikasikia sauti ikiniamrisha tokea nyuma."Simama pale au nikugeuze marehemu wewe kijana".Nikajua pale maji yalikuwa yanataka kunifika shingoni.Sikutaka kujipeleka mikononi mwa wale watu kikondoo kwani nilikuwa nimemwua mmoja wao.Nilijirusha chini na kuanza kutambaa kuelekea kwenye kichaka kilichokuwa hapo karibu haraka sana.Nyuma nikasikia usalama wa bastola ukiondolewa,sauti mfano wa nyuki wakinipita,karibu na sikio la kulia nikausikia.Risasi aliyokuwa amefyatua,mmoja wao,ilinipita sentimita chache na kuichimba ardhi.Mwili wote ukashtuka,mikono ikawa inanitetemeka kama matawi msimu wa vuli.Muda mfupi baadaye utulivu ukarudi eneo lile kando na sauti ya wadudu waliokuwa katika harakati zao ambazo Muumba aliwapa.



    Bila ya kupiga kelele,niliendelea kutambaa huku nikiwa siamini ikiwa nilikuwa hai mpaka muda ule.Nilipofaulu kufika kwenye msitu ule,nilikimbia sana mpaka kwenye barabara kuu.Ilikuwa imefika saa tatu usiku kwenye saa yangu ya mkononi,saa za Afrika mashariki.Nilitembea kando kando ya barabara ile huku mara kadhaa wa kadha nikiangalia nyuma.Sikumtilia shaka yeyote maana niliweza kukutana na watu wachache sana.Magari yote yaliyokuwa yakipita yalikuwa ya kibinafsi na chache sana zikiwa Lori ya kubeba mchanga,kokoto na mawe nami sikutaka kuanguka mtegoni kwani wale watu niliowakimbia nyumbani walikuwa wakitumia gari la kibinafsi.Hili lilinilazimisha kujificha kila niliposikia mngurumo wa gari lolote.Matone ya mvua yalikuwa yakiongezeka muda ulivyokuwa ukisonga.Hali hii ikawa afueni kwangu kwani maji hayo yalikuwa yakisafisha mwili wangu kutokana na uchafu nilipopitia kwenye bomba la choo.



    Nilitembea kwa masaa mawili Kisha nikatafuta pahali chini ya mti,kando ya barabara ile kupumzika kwani nilikuwa nahema kwa nguvu nayo mbavu zilikuwa zikiniuma sana.Mawazo yangu yote yalirudi kwa wazazi wangu waliokuwa,ikiwa ni sahihi kusema marehemu nyumbani kwetu.Machozi yalinitiririka njia nne nne,nikafikiri nipo ndotoni lakini hali ilikuwa halisi.Nikiwa katika fikira nzito,nikakumbuka ufunguo alionipa baba kwa maelezo kwenye barua yake fupi hivyo nikafungua mkoba na kuichukua.Nikaitazama kwa umakini,umbo lake lilikuwa la kawaida ila katikati kulikuwa na mchoro wa mnyama ambaye sikuweza kumjua kutokana na Mimi kutumia hisia za mguso.Giza lilikuwa limeigubika nchi nzima.



    Sikutaka kuchukua muda mrefu pale hivyo niliirudisha funguo ile pahali pake mkobani kisha nikainuka kuendelea na safari yangu ambayo sikujua mwisho wake ungekuwa wapi.Kwa mbali niliona taa za barabarani na za kwenye duka zikiwaka,nikajua karibu nakaribia Mji mkuu wa Sogomo.



    ITAENDELEA

NYUMA YAKO (4) - 5

 





    Simulizi : Nyuma Yako (4)

    Sehemu Ya Tano (5)







    Alihangaika sana lakini hakuna mtu aliyehangaika naye mpaka walipofika mahali walipokuwa wanaelekea, ngome. Humo gari likasimama na Abdulaziz akashushwa na kuzamishwa ndani. Akawekwa kitini na kisha akafunguliwa kinywa sasa.



    “Mtajuta kwa hiki mnachofanya!” akafoka. “Nitawakatakata na kuwatupia simba wangu wa uani!”



    Aliendelea kuropoka na kutoa vitisho. Akijitangazia cheo chake na madara yake lakini hakuna mtu aliyekuwa anahangaika naye zaidi aliambulia kofi alilokandikwa na kitako cha bunduki, akatema damu!



    “Funga bakuli!” Marshall akamwamuru kisha akavuta kiti karibu na mateka wake.



    “Sikia, sina muda wa kupoteza hapa, sawa? Kwahiyo jiepushie maumivu zaidi kwa kunipa ninachokitaka. Sioni shida kukukandika ngumi mpaka uso wake ubadilishe rangi, kwahiyo kuwa na hekima.”



    Abdulaziz akacheka. Kinywa chake kilichokuwa kinatiririsha damu kikamwaga mchuzi zaidi.



    “Wamarekani wote watabusu matako yangu!” akacheka tena kati ya maumivu na kisha akaendelea kutusi basi Marshall akaghafirika na kujikuta akimkanda Abdulaziz ngumi kubwakubwa nzito mpaka mwanaume huyo akapoteza ‘mtandao wa kichwa; kwa muda kidogo.



    “Inatosha Marshall!” Marietta akaingilia. Aliudaka mkono wa Marshall uliokuwa unaendelea kumwadhibu Abdulaziz. “Kwanini tusitumie tu njia nyepesi ya kumnyesha dawa?”



    “Hastahili njia nyepesi huyu mshenzi!” akasema Marshall. Akavuta pumzi ndefu kujipoza kabla hajasonga nyuma.



    Abdul alikuwa anavuja damu nyingi sana usoni. Kwa hali hiyo asingeweza kuongea hivyo basi wakampatia mapumziko kabla ya baadae kumrejea tena.



    Huko ndani na nje ya jiji wanajeshi wakawa wanakatiza huku na kule wakifanya doria. Mara kadha walisimamisha magari na kuwauliza watu maswali kadhaa,hata pia walikuwa wanaingia kwenye baadhi ya makazi ya watu kufanya ukaguzi.



    Lakini hawakuwa wanasema ni nini wanatafuta. Ilikuwa ni siri.



    “Muda umeshafika,” alisema Marshall. “Hatuna muda zaidi wa kungoja, nadhani mnalijua hilo. Hatupo salama hapa.”



    Alikwishakwapua dawa yake mkononi. Basi akamjongea Abdulaziz na kumnywesha kisha akamwamsha. Baada ya kama dakika tano, akaanza kumuuliza bwana huyo maswali. Pasipo kudhamiria, Abdulaziz akajikuta akiweka kila kitu bayana.



    Alieleza wapi ambapo mlengwa wao yupo na yu katika hali gani. Basi baada ya hapo, Marshall pamoja na wenzake wakawa wameshapata wanachotaka lakini bado hawakumwachia Abdul. Wakamweka kwenye gari na kwenda moja kwa moja kule ambapo pameelekezwa.



    Lakini haikuwa rahisi. Mji mzima ulikuwa umetwaliwa na wanajeshi. Walifanya namna ya kukwepa njia kuu lakini bado kazi ilikuwa mbombo ngafu, na ukizingatia wana mwili wa Abdul basi ndo ikawa tabu mara tatu yake.



    Walipotembea kwa kama robo saa wakasimamishwa na wanajeshi kumi waliokuwapo barabarani. Gari likaamriwa liegeshwe kando upesi.



    Mahmoud, ambaye alikuwa ni dereva, akatii amri na kuegesha. Kwenye viti hivyo vya mbele alikuwapo yeye na Kelly tu na huko nyuma hakukuonekana watu. Mahmoud akajitambulisha na pia akamtambulisha Kelly kama mkewe.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Kelly alikuwa amejilaza akionekana hoi. Macho yake yalikuwa yanarembua na kinywa chake kilikuwa wazi. Alikuwa anaonekana amechoka sana, hajiwezi.



    Wanajeshi wakataka kukagua gari.



    “Tafadhali maafisa,” akasema Mahmoud. “mke wangu yu hoi anaumwa. Naombeni nimwahishe hospitali asije akatufia hapa.”



    Alipomaliza kauli yake tu, Kelly akashindwa kujizuia kutapika. Alirushia matapishi kioo cha mbele kana kwamba bomba, hali hiyo ikawashtua wanajeshi ambao walitazamana kwa mshangao. Upesi wakawaruhusu watu hao waende kupata matibabu.



    “Kelly, upo sawa kweli?” aliuliza Mahmoud akiwa amekanyaga pedeli ya mafuta. Gari lilikuwa linanuka sasa.





    **





    Walienda kwa mwendo kidogo kabla ya kusimama kumpa nafasi Kelly. Alikuwa anaumwa. Hakuwa anajisikia vema kabisa. Macho yake yalikuwa yaamelegea na mwili wake umepungukiwa na nguvu.



    “Utaweza kweli kwenda kufanya misheni?” akauliza Marietta akiwa ameuweka mkono wake kwenye bega la Kelly. Mwanamke huyo pamoja na Marshall na Danielle walikuwa wamejificha nyuma ya gari na kufunikwa na shuka jeusi wakati wa ukaguzi.



    Basi baada ya Kelly kujisikia vema wakatoka naye na kwendelea na safari. Mwanamke huyo alisema atajikaza na atakuwa sawa tu. Wakatembea barabarani kwa kama nusu saa kabla ya kufika eneo walilokuwa wamekusudia. Hapo walipoambiwa ndipo kuna mwili wa mlengwa wao.



    Marietta akashusha pumzi akitazama jengo hilo. Aliamini litakuwa ndilo la mwisho kabla ya kumtia machoni mpenziwe. Baada ya kulikagua kwa sekunde kadhaa wakashuka, isipokuwa Mahmoud, sasa wakiwa wamejiandaa kimapambano ya vita. Kila mmoja wao alikuwa amebebelea bunduki.



    Jengo lilikuwa lipo kwenye ulinzi mkali wa wanajeshi kadhaa. Haikuwa inajulikana kwa watu nini wanajeshi hao wanalinda hapo. Ilikuwa ni ‘verified restricted area’. Marshall pamoja na wenzake wakajigawa upanda na kuweka ‘target’ yao katikati, mashambulizi yakaanza.



    Walikuwa vema. Na kwasababu walikuwa ndo wavamizi basi maadui zao hawakuwa wamejiandaa vema kuwapokea. Waliwatupia risasi na kuzama ndani ya eneo baada ya kukata nyaya na sinyenge zilizokuwa zimepachikwa juu ya kuta.



    Wakawatekeza walinzi na kwenda taratibu kwa tahadhari, hatimaye wakazama kabisa ndani, kulikuwa kukubwa, wakagawana mwelekeo kila mtu akienda na njia yake. Ndani ya muda mfupi wakawa wamewateketeza walinzi karibia wote ingali wao wakiwa salama salmini.



    “Ni lile lango!” akasema Marietta akinyooshea kidole upande wao wa mashariki. Wakasonga huko kwenda kukutana na chumba kilichozibwa na mlango mkubwa wa chuma. Hapo ikawapasa wapate namna ya kuzama humo. Mlango ulikuwa unafunguliwa na alama ya kidole.



    “Tumtumie huyo mlinzi!” bwana Marshall akapendekeza akiwa anamtazama mlinzi aliyekuwa amelala mfu kwa pembeni yao.





    **

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/



    “Mkuu, unadhani watakuwa wapi?” aliuliza mwanajeshi akimtazama bwana Masoud. “Tumetafuta kwa masaa sasa lakini hamna mrejesho.”



    Masoud alikuwa ametulia kwa mawazo. Alikuwa anatafakari mambo kichwani. Kidogo wazo kubwa likamjia na kuwaamuru wanajeshi wake wote waongozane naye. Bwana huyo aliwaza kama wamarekani watakuwa wamemteka bwana Abdul basi watakuwa wamempeka wapi?



    Moja kwa moja mawazo yake yakaelekea kule kulipokuwa na mateka wao - mateka wa Abdulaziz. Wamarekani hao watakuwa wanataka kumkomboa mtu wao kisha watoroke.



    Basi magari pamoja na pia helikopta za kijeshi yakaelekea huko kwa wingi. Vyote vilikuwa kwenye mwendokasi mkubwa.



    **



    “Upesi! Upesi!” Marshall alisihi. Mwanume huyo alikuwa amemweka mtu mongoni akiwa ana ‘trot’, nyuma yake alikuwapo Marietta, Danielle na Kelly.



    Watu hao walikimbia mpaka kufikia mahali Mahmoud alipoegesha gari. Mahmoud alipoona wenzake naye upesi akashuka kusaidizana na Marshall. Wakauweka mwili aliokuwa ameubeba Marshall mgongoni alafu wakajipaki garini.



    “Yu mzima?” Mahmoud akauliza.



    “Ndio, ila yupo hoi sana!” akajibu Marshall. Gari likatimka na wasifike mbali mara taa kubwa ikawamulika tokea juu. Tayari helikopta za kijeshi zilikuwa zimewasili. Isichukue muda, risasi zikaanza kutupwa kufuata gari hilo. Kwakuwa risasi zilikuwa zinatoka juu basi zilikuwa kana kwamba mvua.



    “Usifyatue risasi hovyo!” Masoud akapaza kwenye ‘radio call’. Yeye alikuwa kwenye gari linaloenda kwa kasi. “Labda Abdulaziz yupo humo, usifyatue risasi kwa fujoo!”



    Basi baada ya amri hiyo risasi zikaacha kutupwa na helikopta mbili sasa kwa idadi zikawa zinawafukuzia wakina Marshall kimyakimya. Magari nayo yalikuwawa yanasogea kwa ukaribu zaidi.



    “Sasa tunafanyaje?” akauliza Kelly. Mambo hayakuwa mambo kabisa. Usalama wao ulikuwa hatarini. Ni kama vile kila mtu alikuwa ameshikwa na kigugumizi.



    “Yatupasa tuwashambulie,” akasema Marshall. Kwake hakuona kama kuna njia mbadala kwani maadui walikuwa wanawasogelea zaidi.”Bwana Mahmoud mpatie Danielle usukunai tafadhali, sisi wengine yatupasa tupambane sasa.”



    “Lakini tutawezaje kupambana na watu wengi vivyo?” Marietta akauliza. Uso wake ulikuwa umejawa na shaka. Danielle akamtazama na kumwambia itakuwa rahisi kufanya vivyo tofauti kabisa na mawazo yao kwani wale wanajeshi watakuwa wanahofia kuwashambulia.



    “Kwanini?” Marietta akauliza.



    “Kwasababu Abdulaziz yupo humu. Kama hawajui basi tuwajuze hilo,” Danielle akatoa maelezo. Punde akakabia usukani na Marshall akapasua kioo cha nyuma na kuonyeshea mwili wa Abdulaziz. Sababu mwanga wa helikopta ulikuwa mkubwa hivyo mwili ulionekana vema.



    “Mkuu, mwili wa Abdulaziz upo ndani ya gari! Upo ndani ya gari, over!” alisema bwana aliyekuwapo kwenye helikopta, basi bwana Masoud akata agizo gari hillo lisishambuliwe ili kuulinda usalama wa kiongozi wao.



    Lakini kinyume na matarajio yao, wakaanza kushambuliwa na wakina Marshall. Kwa ustadi kabisa bwana Marshall akazidungua helikopta zote mbili kwa risasi nne tu! Helikopta ziliyumbayumba na kugongana na kisha kuangukia magari yaliyokuwa yanaongozana nayo. Magari matatu yakalipuka papo apo, na matatu yakavamiana na kugongana vibaya.



    “Tazama! Tazama!” Masoud alibwatuka kumwonyesha dereva wake kigingi cha gari mbele yao. Dereva alikikwepa wakaendelea kusonga mbele. Ni magari nane tu ndo yalifanikiwa kutoka salama na kuendelea kuwafukuza wakina Marshall.



    Nayo magari hayo yakakumbana na shurba za risasi haswa. Marshall, Kelly na Mahmoud walikuwa wanatumia risasi zao vema kufyatua na kubangua. Walichokuwa wanakifanya ni wengine wakiwa wanelenga vioo vya magari, Marshall yeye alikuwa analenga sehemu za kuhifadhia mafuta.



    Kila alipotupa risasi mbili alikuwa anaangusha gari. Muda si mfupi, yakabakia magari mawili tu yakiwa yanazungusha matairi.



    Bwana Marshall akatoa kurunzi kubwa iliyokuwapo nyuma ya gari, akawamulika wale waliokuwa wanawafuata na kuwafanya wapoteze mwelekeo kabisa. Madereva hawakuweza kumudu mwanga mkali wa kurunzi, basi wengine wakagongana na kuumizana.



    Dereva aliyekuwa anamwendesha bwana Masoud yeye akasimamisha gari kwa usalama. Zaidi Risasi zikatupwa kutoboa kioo cha gari hilo na kummaliza dereva mara moja. Ni kheri bwana Masoud yeye aliwahi kuinama na kujiweka salama zaidi.



    Baadae Masoud alipokuja kuamka, hakuweza tena kuendelea. Alikuwa ameshindwa. Hakuamini macho yake alipotazama kando na nyuma yake, watu walikuwa wamejeruhiwa vibaya hata kufa. Alikuwa amepoteza wapambanaji wengi sana.



    Kwa hasira akapaza sauti kuu atoe mzigo wa ghafira kifuani mwake.





    **



    Bada ya masaa manne…





    “Ngoja tuone,” alisema Danielle. “Nadhani ataamka.”



    Mwanamke huyo alikuwa ametoka kumtazama mlengwa wao waliyetoka kumwokoa. Kwasababu alikuwa ana taaluma hafifu ya mambo ya uuguzi, alitumia karama hiyo. Mlengwa wao alikuwa amekonda sana, afya yake ilikuwa imedorora kweli. Ni wazi alikuwa hapewi chakula ama basi hakuwa anakula kwa kusudi.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Kumtazama ilikuwa yataka moyo.



    “Itachukua muda gani kuamka?” Mariett akauliza.



    “Sijajua. Tumpe muda kidogo. Mwili wake ulikuwa na upungufu wa maji sana,” Danielle akaeleza. Basi baada ya muda kidogo, kweli, mgonjwa akaamka. Basi kwanza Marietta akapewa nafasi ya kwenda kuonana na kuongea na mumewe kabla ya yeyote.



    Ikapita kama dakika kumi, mara Marietta akatoka ndani ya chumba na kuja kukutana na wenziwe. Uso wake ulikuwa na tembe za shaka.



    “Hakumbuki kitu,” akasema mwanamke huyo. “hakumbuki chochote. Si mimi wala si Marekani. Hamna kitu anajua!” Marietta akaanza kulia.





    Ilikuwa ni ajabu kidogo, kwa uhakiki Marshall na pia Danielle wakaenda kumwona mlengwa wao. Na kweli wakagundua hakuwa na kumbukumbu yoyote ile! Kila mtu kwake alikuwa mgeni asiyemtambua!

    "Huenda wakawa wamempatia madawa?" Marietta akauliza. Alikuwa na hofu. Vipi kama mumewe hatokumbuka tena kitu milele yake? Atakuwa vivyo mpaka lini?

    Walifikiri na hakukuwa na namna ya kufanya isipokuwa tu sasa wafikirie kumsafirisha bwana huyo kwenda Marekani. Huko kwa ubora wa tiba lakini pia kwa nafasi yake atapata huduma upesi na kurejea kwenye hali yake.

    Lakini ni wazi hilo halikuwa jambo jepesi hata kidogo. Ni katika siku hiyohiyo nyakati za usiku, wakasikia geti likigongwa kwanguvu. Walikuwa ni wanajeshi wa doria!

    Upesi walitoka ndani ya eneo kwa kuuruka ukuta. Marshall alikuwa amemweka mume wa Marietta mgongoni mwake, ingali Mahmoud yeye alikuwa amebebelea mwili wa Abdulazizi. Hawakuwa wanauacha maana ulikuwa muhimu sana kwenye swala la usalama.

    Walipotua upande wa pili, wakakimbia lakini wasifike mbali milio mingi ya risasi ikaanza kuwafuata. Ni Mahmoud ndiye alikuwa amekaa kwa nyuma akiwa amembeba Abdulaziz.

    Mwanaume huyo alitifuliwa risasi ya mguu akapiga yowe kali la maumivu. Kabla hajasaidiwa, zikatupwa tena risasi mbili lakini kheri hazikumpata na badala yake zikazama kwenye mwili wa Abdulaziz!

    Upesi Danielle akasimamisha gari kwa kutumia tundu la bunduki kisha wakakwea humo watimke. Mahmoud alijikongoja kufuata gari walilozama wenziwe, lakini asitimize adhma, akatunguliwa risasi ya kichwa!

    Mahmoud alikuwa amefia papo hapo asiombe hata maji. Kwakuwa alishafika karibu na gari, Marshall akafanya jitihada kuvuta mwili wa Mahmoud pamoja pia na wa Abdulaziz huku gari likienda zake.

    Gari likashambuliwa sana na risasi. Nalo lilipoenda kwa kama umbali wa wa robo kilometa tu, ajabu likatokea gari kubwa upande wao wa kushoto na kuwabamiza kwa mbele. PUUH!!

    Gari lilikuwa limechakaa. Mbele kwenye boneti palikuwa panafuka moshi mzito na panakoroma! Pamefunuka na kupindapinda.

    Waliokuwemo ndani; Marshall, Marietta, Kelly, Jack na Danielle, walikuwa hoi kwa maumivu lakini wakiwa wazima. Danielle aliyekuwa ndiye mshika usukani yeye alikuwa anavuja damu kichwani, si kwa wingi sana.

    Ni kheri gali hilo halikuwa limebamiza walipokuwa wameketi bali tu sehemu ile ya mbele.

    Basi Danielle akarudisha gari nyuma na kulitengenezea kisha akalikimbiza kwa fujo kana kwamba ni jipya toka kiwandani. Tairi la kushoto la mbele lilikuwa linaonekana lote mpaka na shina zake zilizoshikilia.

    Hapa ndo' Danielle akaonyesha umwamba wake kwenye usukani. Akaonyesha dhahiri kwanini bwana Marshall anapendelea kumpatia nafasi ya kushika usukani.

    Alitimua haswa kuelekea baharini. Wale waliokuwa wanamfukuza wakapata changamoto haswa kumtia nguvuni. Mwanamke huyo alikuwa anacheza na magari mengine barabarani akiyasukuma ama kuyachokoza kama anayagonga ili apate kuwaziba wanaomfuata.

    Kwenye kona alikuwa mahiri kwa kwenda mzima pasipo kukanyaga pedeli ya breki, na pia alikuwa mashuhuri kwenye kuyakwepa magari barabarani kwa ustadi.

    Ndani ya nusu saa, akawa ameshawaacha kabisa walokuwa wanamkimbiza. Akatimba baharini na huko wakateka boti kubwa ya kutorokea.

    "Hii itatuondoa hapa upesi!" Akasema Marshall.

    Basi akaiwasha lakini kabla hajaondoka akastaajabu kumwona Marietta na Kelly wakiwa wamesimama upande mmoja wakiwatazama. Kufumba na kufumbua Marietta akawanyooshea bunduki na kuwaambia,

    "Safari imeishia hapa! Nashukuruni kwa kila kitu."

    Marshall akamtazama Danielle na kisha Jack. Wote walikuwa wamepigwa na bumbuwazi. Hawakuwa wanaamini kile kilichokuwa kinatukia mbele ya macho yao.

    Basi kwakuwa walikuwa wameonyeshewa silaha, hawakuwa na ujanja. Wote wakanyoosha mikono juu na kutii. Marietta akawataka waende nje na kujitupia majini.

    Taratibu wakasonga, kabla hawajafikia mlango, sauti ya koki ya bunduki ikaita. Kutazama alikuwa ni Kelly. Mwanamke huyo alikuwa amemnyooshea Marietta bunduki kichwani.

    "Weka silaha chini!" Akafoka.

    "Kelly!" Marietta akastaajabu. Alitoa macho ya woga na mashaka.

    "Weka silaha chini sasa hivi!"

    "Kwanini unafanya hivi?" Marietta akauliza.

    "Nina mimba ya Jack. Mtoto wangu hawezi kuwa yatima. Ni hivyo."

    Marietta akang'ata meno yake kwanguvu. Akajilaumu kwanini hakufikiria kuhusu hilo swala mara zote vile alipokuwa anamwona Kelly akihangaika.

    Akajiona mjinga.

    Lakini hakutaka kutii amri. Hakutaka kushindwa. Aliamishis mkono wake wenye silaha kwa Kelly lakini asiwe mwepesi vya kutosha , Kelly akamuwahi na kumshindilia risasi ya bega!

    Asiridhike, akataka kufurukuta tena, sasa ikamlazimu Kelly atumie risasi nyingine kumkalisha. Risasi hiyo ilitoboa shingo ya Marietta na kumlaza mwanamke huyo akiwa hoi bin' taaban chini.

    Anavuja damu kupita kiasi. Mkono wake wa kuume ulokuwa umebebelea bunduki sasa umeshikilia jeraha lake.http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Japo alikuwa ni mdhalimu, alitia huruma. Kinywa chake kilikuwa kinatema damu nyingi kwa mtindo wa kwikwi! Kidogo akakata pumzi.

    Watu wote walikuwa wanamtazama wakijawa na maswali. Hawakuwa na cha kufanya kumsaidia.

    "Mmezungukwa na wanausalama!" Mara wakasikia sauti toka kwenye kipaza. "Wasilisheni silaha zenu na mtoke mikono ikiwa hewani!" Sauti ilinguruma. Kweli walipotazama wakapata kuona wakiwa wamezingirwa na boti tatu na ufukweni kuna watu kadhaa wakiwa wamenyooshea bunduki zao kwao.

    Tangazo likarudiwa tena. Mara hii msemaji akasema kwamba hatorudia tena maneno yake kabla hajaruhusu risasi zimwagike hewani!

    "Sasa tunafanyaje?" Kelly akauliza. Jack akamtazama mwanamke huyo na kusema, "ni kweli una mimba yangu?"

    "Ndio!" Kelly akajibu.

    Jack akamsogelea karibu Kelly na kumkumbatia. Alifurahi kusikia habari hiyo japo muda haukuwa sahihi. Angetamani aonane zaidi na Kelly lakini pia na mtoto wao lakini ni wazi muda haukuwa upande wao.

    Kitendo hicho kikamgusa Marshall katika namna ya kipekee. Alikuwa amechoka kumwona Jack akiwa hana furaha mbele ya macho yake. Hakuwa radhi hali hiyo iendelee.

    Kichwani mwake aliamini, nafasi ya kuchoropoka hapo ilikuwapo. Ndio ni ngumu lakini ipo.

    "Moja!" Sauti ikavuma toka kwenye kipaza. Wanajeshi wote walikuwa wamejiandaa kushambulia.

    Marshall alitazama pande zote nane za dunia. Akapiga mahesabu yake kichwani juu ya namna watakavyopata salama. Ilikuwa ni ndani ya sekunde tatu tu.

    Mara akaropoka, "laleni chini!" Kisha akalitimua boti kwa fujo kufuata boti moja ya wanajeshi. Alipoikaribia akakata kona kali kuibamiza kwa ubavu, alafu akatokome alipopata njia. Huko nyuma risasi zikiwafuata kana kwamba mvua.



    **



    Baada ya lisaa limoja ...



    "Tumeipata. Over! Tumeipata boti, over!" Alisema mwanaume mmoja ndani ya boti ya kijeshi. Mbele ya macho yake kulikuwa na boti kubwa. Boti ambayo ilitumiwa na wakina Marshall kumtimikia.

    Basi wakaijongea boti hiyo na kuikagua. Muda si mrefu zikafika hapo boti zingine nne zenye kubebelea wanajeshi. Walipotazama ndani wakapata kukuta mwili wa Abdulaziz. Tayari ulikuwa mfu.

    Mbali na hapo hakukuwa na mwili mwingine isipokuwa kutapakaa kwa damu. Walitafuta boti nzima wasione jambo. Sasa Marshall na wenzake walikuwa wapi?

    "Hamjawaona?" Sauti ikauliza kwenye radio call.

    "Hapana mkuu. Kuna maiti ya Abdul pekee, over!"

    Wakati huo kwenye masafa ya maji umbali kabisa na nchi ya Morocco, Marshall alikuwa ameketi kwenye kiti cha mbele cha boti. Mkono wake ulikuwa umebebelea kinywaji kwenye glasi na pembeni yake alikuwa ameketi bwana James Peak.

    Bwana huyo alikuwa amevalia suti yake maridadi kabisa, naye mkononi alikuwa amebebelea glasi yenye kinywaji. Huko nje kulikuwa na makomando waliokuwa wamebebelea bunduki wakitazama usalama.

    Boti hiyo ilikuwa na chapa ya bendera ya Marekani ubavuni mwake.

    "Ulijuaje yote haya?" Akauliza Marshall akimtazama James. Kwanza James akatabasamu,

    "Kila mtu anajua ulimwenguni kinachoendelea Morocco. Unadhani nisingefahamu na Marietta alikuwa ameelekea huku? Nalijua nanyi mtakuwapo. Ian amenieleza mengi sana."

    "Na vipi ukapewa vyote hivi na serikali?"

    "Sababu ya vielelezo vya Ian na vyangu pia. Anyways, mimi sikuwa polisi mpelelezi tu kama ulivyokuwa unajua wewe."

    Marshall hakuuliza tena. Alitaka tu kupumzika hivi sasa. Alimuaga James na kwenda zake ndani kukutana na wenziwe. Haikuwa rahisi kabisa. Hata alipowaona wakiwa hai alipata kufurahi sana moyoni mwake.

    Hakika ilikuwa ni misheni ya aina yake.



    **



    Baada ya mwezi mmoja ...

    "Anaendeleaje kwa sasa?"

    "Yu vema."

    "Amerejesha kumbukumbuze?" Marshall akauliza tena.

    "Kwa kiasi kikubwa. Kadiri anavyokaa na mwanaye maendeleo yake hushamiri. Muda si mrefu atakuwa na uwezo wa kueleza kila kitu."

    "Nashukuru, James."

    "Hillton. Ni bwana Hillton, Marshall."

    "Hilo la James limekaa sana. Itachukua muda kidogo kulifuta. Anyways, nashukuru na uwe na siku njema."http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Marshall akakata simu na kwenda kujumuika na wenzake. Alimkumbatia Danielle akambusu kisha akamtaka Jack apandishe sauti ya muziki.

    "Huoni itamwathiri mtoto wangu?" Jack akauliza akishika tumbo la Kelly. Wote wakajikuta wakicheka.

    "Jack," Danielle akaita na kuuliza, "hautaki tumfuatilie tena yule mwingine na bwana wake?"

    Jack akakunja sura. Wote wakacheka tena.



    **



    MWISHO

Blog