Search This Blog

Sunday 20 November 2022

NJIA NYEMBAMBA (2) - 2





      Simulizi : Njia Nyembamba (2)

      Sehemu Ya Pili (2)







      Ni saa moja asubuhi na inamkuta Kone akiwa macho kwa kukosa usingizi. Anafungua pazia la dirisha lake kutazama nje, jua limesha amka. Haamini kwani anaona usiku umeenda haraka mno akiwa mpweke.

      Macho yake ni mekundu mno. Amevalia suruali ya kitambaa na mkanda wake. Chumba kipo hovyo; si viatu wala soksi kilikuwa mahala pake.

      Alinyoosha mkono wake kuupeleka kaskazini mwa kitanda akatafuta tafuta kitu, hakufanikiwa. Aliupeleka kusini akaikumba simu yake aliyoipeleka usoni na kutafuta jina la Rose. Alimpigia mwanamke huyo kisha akaiweka simu sikioni. Simu iliita mara tatu, ikapokelewa.

      Alimuuliza juu ya hali ya Kessy, Rose akamtaarifu na kumpasha yote mpaka ya Talib.

      “Raisi haniamini tena. Hataki kuniona na amesema ataendelea na vile yeye alivyopanga,” alilalama Kone. “Sijui cha kufanya kwa sasa, Rose. Nimechanganyikiwa kwakweli.”

      “Usijali,” Rose alimpa moyo. “Nakuhakikishia Kessy atakufa si zaidi ya siku mbili.”

      “Nimeshazoea ahadi, Rose. Raisi hataki tena ahadi!”

      “Hii siyo tena ahadi bali ni uhalisia,” sauti ya Rose ilitamba, kisha: “Ngoja ntakupigia baadae, kuna kazi nafanya.”

      Alisema hivyo na simu ikakata.

      Kone alishusha pumzi ndefu, akalaza kichwa chake juu ya kitanda. Alitazama dari kwa muda kidogo, mara ghafla akasikia honi ya gari huko nje. Alinyanyuka upesi akakimbilia huko mithili ya mwehu. Alijua ni Fatma anarejea, na sasa alikuwa anataka kumuona huyo mwanaume anayemleta kila siku.

      Alifikia geti akalikuta limefungwa. Alimkurupusha mlinzi ndani ya kibanda chake na kumtaka afungue geti upesi. Mlinzi alifanya hivyo, Kone akatoka nje. Huko alikutana na Fatma uso kwa uso na gari lililomleta likiwa bado halijaondoka. Lilikuwa ni lile lile, Prado, alilowahi kuambiwa na mlinzi.

      Alilikimbilia apate kumwona mwanaume anayemharibia mkewe. Alipofika kwenye vioo vya mbele vya gari akamwona mwanaume rangi ya kahawia akiwa amevalia shati la bluu na tai nyeusi. Alikuwa ameshikilia usukani na punde tu alipomuona Kone alikanyagia mafuta akatimka.

      Mwanaume huyo alikuwa mgeni kwa Kone, hakuweza kumtambua kabisa. Alivuta kumbukumbu yake ikagoma. Alichoweza kukifanya ni kunakili namba ya usajili ya gari na kisha akageuka kumtazama mkewe, hakumuona. Alikuwa tayari ameshazama ndani.

      Haraka alifuata geti akajaribu kufungua, akashindwa. Lilikuwa limefungwa kwa ndani. Alimwita mlinzi na kumwamuru amfungulie, mlinzi akamtaarifu ya kwamba mkewe, Bi Fatma, ameondoka na funguo kwenda nazo ndani. Kone akapandwa na hasira maradufu. Ulikuwa ni muda wake sasa wa kutumia ujuzi wake aliojifunza jeshini miaka kumi na tano iiyopita; alikwea uzio kama nyani akajitupia ndani.

      “Sasa twatiana vidole puani!” Alifoka na nafsi.

      Alitembea haraka kwenda ndani na baada ya muda mfupi sauti ya kuvunjwa mlango iliita, na mara ikafuatiwa na ya kilio cha mwanamke. Sauti hiyo ilidumu kwa dakika tano tu na mara ikawa kimya, tena kwa ghafla.

      Bi Fatma alikuwa amepoteza fahamu!



      Masaa kumi baadae, Sierra Leone:



      Bado giza halikuwa limeingia japokuwa mwanga wa jua tayari ulishakuwa hafifu. Kwa muda ilikuwa ni saa kumi na moja jioni iendayo kwenye kumi na mbili wakati gari lililombebelea Talib likifika kwenye uwanja wa hospitali likiongozwa na msafara wa magari manne.

      Talib, aliyekuwa amevalia shati na suruali nyeusi, alitoka garini akatembea kuingia ndani ya hospitali akisindikizwa na mlinzi mmoja mwenye mwili mpana ndani ya suti. Safari yake hiyo ilikomea mbele ya mlango wa chumba alicholazwa Kessy ambapo aliwakuta wanajeshi wawili waliobebelea mitutu ya bunduki.

      Wanajeshi walimsalimu mkuu wao kisha wakamruhusu kuingia ndani. Talib aliketi pembeni ya kitanda alicholazwa Kessy, akamtazama mgonjwa huyo kwa uso wa masikitiko. Sura ya Kessy ilikuwa nyeusi kana kwamba imevujia damu. Alikuwa amevimba kama kitumbua kiasi kwamba unaweza usimtambue. Kwa kumuona ungeweza kumsamehe yale yote aliyoyatenda huko nyuma.

      Talib hakusema kitu kwa muda wa kama dakika mbili. Alikuwa anamtazama tu Kessy. Ila mwishowe alivuja chozi pale alipotwaa mto uliokuwepo kitandani. Alimvua Kessy kinyago cha kuhemea kisha akamfunika na mto aliombania nao kwanguvu mpaka pale Kessy alipotulia tuli kuashiria amekufa.

      Talib alishusha pumzi ndefu, akasema:

      “Samahani Kessy. Ni wakati wangu sasa.”





      Talib alishusha pumzi ndefu, akasema:

      “Samahani Kessy. Ni wakati wangu sasa.”

      Baada ya muda mfupi akiwa anamtazama Kessy ambaye sasa alikuwa marehemu, alijikuta anatabasamu. Alijihisi sasa amekuwa kipepeo toka kwenye muundo wa dudu washa. Alijihisi amekuwa mwepesi kama unyoya lakini kwa wakati huo akiwa mwenye kujawa nguvu na madaraka.

      Alah! Ati Talib alikuwa amekufa. Kifua chake kilichobebelea chuki kilikua kimetuama. Ndio alikuwa amekufa. Hilo halikuwa na pingamizi tena, alienda na ngebe zake.



      ***



      Kinyume na yalivyokuwa matarajio ya wengi, msiba wa Kessy ulidumu kwa siku mbili tu. Viongozi wachache sana waliudhuria tena toka mbali, wengi wao waliishia kutoa salamu za rambirambi ama kunyamaza kabisa ikiwemo Guinea. Lakini kilichoshangaza zaidi ni kwamba hata basi Al Saed wa Liberia naye? Hakufika! Ni wazi kulikuwa kuna jambo, hili lilitatiza raia ingawa hawakuwa wanampenda kabisa Kessy. Na kwa namna moja ama nyingine, Talib akatumia hii fursa kutimiza haja.

      “Habari zenu wananachi wa taifa kubwa la Sierra Leone,” ilikuwa sauti ya Talib ikitokea kwenye spika za redio, na kwa wale wenye televisheni wakapata kumuona kabisa kiongozi huyo kwenye chaneli ya taifa akiwa amevalia sare za jeshi zilizopambwa na ‘vidudedude’ vingi vinavyong’aa. Alikuwa na uso wa tanzia lakini mkakamavu.

      Watu walivutika kumwona na hata kumtazama. Kila mmoja alikuwa anataka kujua hatma ya nchi, lakini zaidi juu ya kifo cha Kessy ambacho kiligubikwa na utata na wingi wa siri. Walitumai watapata majibu ya maswali yao yaliyotuama kichwani hivyo wakaandaa macho pamoja na masikio.

      Talib alijua kiu hiyo, na basi tokea alipoanza kuhororoja akawa anakuna pale panapowasha. Lakini si kwa kucha kama vile ambavyo wasikilizaji na watazamaji walidhani, bali kwa chuma! Alijaza uongo na pumba za kulaghai akiwa anajimiminia sifa kedekede. Ila zaidi alijenga uhasama baina ya nchi yake na mataifa mengine, haswa jirani.

      “Inasikitisha sana kusema ya kwamba, kiongozi wetu mkuu aliuawa na rafiki yake kabisa, bwana Al Saed, ambaye alimtilia sumu walipoonana mara ya mwisho katika jiji la Freetown kwa ajili ya kujadili mambo kadha wa kadha ya maendeleo. Na kwa matokeo yake, jirani yetu huyo ameona aibu hata kufika kwenye msiba, amebakia kujificha nyumbani kwake. Inashangaza sana hili maana hamna taarifa rejeshi yoyote inayoonyesha kama walikuwa na mtofautiano wa mawazo.”

      Hapa kwa wale waliokuwa mbali na vyombo vya taarifa ya habari wakajisogeza karibu zaidi. Lilikuwa linasisimua hili.

      “Inasononesha kuona pia hata jirani yetu, Guinea, nao wameamua kuonyesha unafki wao hadharani kwa kutojihusisha kwa namna yoyote kwenye msiba wa kiongozi wetu. Ni vema, na tunampongeza kwa kuweka wazi ngozi yake ya chui. Lakini aishi akifahamu ya kwamba atakapobanwa na kiu, ni sisi wa karibu ndio tutakaomhudumia.”

      Hakukomea hapo, akajinadi mbele ya wananchi.

      “Wale waliodhani ya kwamba Sierra Leone itatetereka baada ya kumuua kiongozi wetu, basi wamejidanganya, tena sana. Nataka kuwahakikishia wananchi wote wa Sierra Leone usalama wa kuaminika kabisa, nchi yetu haitotetereka kwa namna yoyote ile, wala hakuna yeyote atakayehatarisha usalama wetu. Tumejipanga kwenye mipaka yetu yote na tupo tayari kwa wakati wowote kumwaga damu kwa ajili ya nchi yetu.”http://pseudepigraphas.blogspot.com/

      Hapo uso wake ulionekana kusahau tanzia, ukachanua tabasamu kwa mbali. Ni kwa mtazamaji makini ndiye angeligundua hilo.

      “Kwanzia sasa nchi itakuwa chini ya wizara ya ulinzi, na ningechukua hii fursa kutangaza safu mpya ya uongozi. Naamini kabisa kwa kushirikiana na hawa watu tutahakikisha ufanisi kwenye kuendesha nchi yetu.”

      Sasa hapo akashindwa kuzuia kabisa tambazo la furaha kwenye paji lake la uso. Aliwataja watu kumi na mbili akiwagawia nyadhifa mbalimbali, watu hao wote wakitokea kwenye jeshi la Sierra Leone. Lakini kaba hajafunga mjadala huo wa madaraka, akamtaja na bibie Rose. Haikuwashangaza wanachi kwani hawakuwa wanamjua Rose, ila lilimshangaza Rose mwenyewe. Karibia litoe moyo wake nje ya kifua!

      Katibu mkuu wa nchi! Si cheo kidogo. Rose alijihisi kichwa chake ni chepesi kulinganisha na majukumu aliyotwikwa. Lakini bado tabasamu lilimjaa usoni, pia na hofu ndaniye.

      Alitaka kumshirikisha mtu furaha yake hiyo, na hakuwepo yeyote isipokuwa Kone. Alimtafuta mwanaume huyo simuni lakini hakumpata, mpaka pale alipojaribu mara tatu. Kiu chake kilikuwa kikubwa na hakuweza kutunza furaha yake kifuani.

      “Unasema kweli?” Aliuliza Kone. Sauti yake ilikuwa ya kukoroma usipate shida kujua ametoka usingizini.

      Rose alijinasibu juu ya bahati yake hiyo, lakini hakuchukua muda mrefu akagundua Kone hakuwa sawa. Mwanaume huyo alikuwa anajitahidi kuficha hali yake, ila haikutosha kumfanya Rose asing’amue kuwa mwanaume huyo yu matatizoni.

      “Mke wangu yupo hospitali. Sijisikii vizuri kabisa, maisha yangu yapo mrama,” alieleza Kone. Macho yake yalikuwa mekundu. Hakuwa nadhifu kabisa.

      Rose alimpatia pole. Alikata simu baada ya kuona Talib anampigia, lakini aliahidi kumtafuta tena Kone baada ya kumaliza kuongea.

      Hivyo akatimiza ahadi baada ya dakika tatu.

      “Amesema tutaapishwa keshokutwa. Nadhani kesho nitakuja kukuona huko Guinea lakini itakuwa siri sana. sitaki afahamu kabisa kama nina mahusiano na Guinea,” Rose alisema. Kone aliafiki mpango huo.

      “Najua una mawazo fulanifulani kichwani. Si salama kuongelea kwenye simu bali uso kwa uso,” aliendelea kueleza Rose. Napo Kone akaafiki na simu ikakatwa.

      Alirudisha simu mfukoni mwake akashika tama. Alikuwa kwenye hospitali kubwa kwa ajili ya kumjulia hali mkewe. Nafsi yake ilikuwa inajuta kwanini alimshushia kipondo bi Fatma kiasi kile. Alijuta kwanini hakuweza kumudu hasira zake. Alijiona mpumbavu, na baba asiyestahili. Lakini alikuwa na maswali mengi kichwani juu ya Fatma. Alikuwa anataka majibu, bahati mbaya hakuwepo pale kumjibu.

      Aliwaza na kuwazua. Aliona ana haja ya kwenda kwa Raisi kumpa taarifa juu ya kifo cha Kessy. Ndio, aliona hilo ni sahihi kwa muda huo. Alifikicha macho yake akasimama.

      Usiku mzima hakuwa amelala vema kutokana na mbu wa hospitali. Muda pekee aliopata wa kulala ilikuwa ni pale alipoegemea kiganja chake cha mkono wa kuume ama kushoto. Hakuweza pia kufanya hivyo kwa muda mrefu, zaidi dakika tano.

      Alipopiga hatua tatu tu, simu yake iliita; alikuwa ni Raisi. Aliipokea simu hiyo haraka akaiweka sikioni.

      “Ndio nilikuwa nina mpango wa kuja huko, mheshimiwa.” Aliikarimu simu kwa maneno hayo. Raisi alisafisha koo lake, akasema:

      “Nahitaji uende Sierra Leone haraka iwezekanavyo.” Sauti ilikuwa kavu na usingehitaji kuelezewa kujua ya kwamba ilimaanisha kile kilichotamkwa.

      “Huu ndio muda wa wewe kutazama fursa ya kutimiza kile tulichokiazimia kabla serikali hii haijatengemaa,” aliendelea kusema Raisi.

      Kone alitabasamu, kisha naye akasema:

      “Hakuna shida mkuu. Ila hatuna haja ya haraka kwa sasa kwani Rose, yule mdada niliyekuwa naye pamoja, ni mmoja wa watu walioteuliwa, tena kuwa katibu mkuu wa nchi! Hivyo hatuna tena haja ya papara.”

      “Rose anihusu, Kone. Wewe ndiye mwenye hii kazi na si mwinginewe,” alisema Raisi. Kone tabasamu likajiminya.

      “Nimesema haraka iwezekanavyo. Nadhani tumeelewana,” Raisi alisema kisha simu ikakata.

      Kone alikosa cha kufanya kwa muda wa dakika mbili; alikuwa amesimama kama mnara. Alishika kiuno akitazama chini. Mwishowe alirudi kwenye viti vya hospitali akaketi na kushika tama.

      Mwanaume ameumbwa mateso, lakini aliona sasa yamezidi. Aliona sasa ulimwengu unamuonea. Awali alikuwa anatamani Kessy afe basi amalize kazi, tayari amekufa, bado tena yaja kazi nyingine! Kufa kwa Kessy kwake kulikuwa kuna maana sana, si kwamba Raisi wake atapata anachokitaka, la hasha! Bali atapata muda wa kuketi na familia yake.

      Sasa nayo ndoto yake ilikuwa inayoyoma. Alihisi moyo wake unasagwa kuwa chapati. Kama isingelikuwa jicho la mwanaume ni gumu kupokea chozi, basi angelikuwa tayari ameshabubujika. Alimfikiria mkewe na hali yake ile. Aliwafikiria wanawe na hivi hawana mzazi wa kuwatazama. Alikumbuka sauti ya mkewe ikimuonya dhidi ya mpango huo awali kabisa. Akajikuta anasaga meno.

      Alibadilisha kila aina ya tama akachoka. Alizinduliwa na mtetemo wa ujumbe mfupi kwenye simu yake. Alitoa simu yake akatazama. Ulikuwa ni ujumbe toka kwa Raisi. Kone alitikisa kichwa akiufungua apate kuusoma.

      “Pesa tayari imeshaingizwa kwenye akaunti yako. Fanya ulichoagizwa.”

      Ujumbe ulisomeka hivyo.

      Kwa hasira, Kone alibamiza simu sakafuni.



      ***



      Ndani ya Toyota Prado nyeusi yenye vioo visivyoonyesha ndani.



      Samweli, msimamizi mkuu wa ulinzi Liberia, alikuwa pamoja na wanaume wawili waliovalia kiraia. Wanaume hao walikuwa wanamtazama Samweli kwa umakini akiwapa maelezo juu ya nini cha kufanya. Walikuwa ndani ya eneo lijulikanalo kama Pleebo, ndani ya kata kubwa ya Maryland, kusini mwa nchi ya Liberia. Eneo ambalo kwa mujibu wa msimamizi wa ulinzi, bwana Samweli, lilikuwa linahisiwa kuwafadhili kundi changa la AMAA – Alwaqt min ajil alttaharrur.

      Walitakiwa kuwa waangalifu sana kwenye eneo hilo lenye udongo mwekundu ndio maana wakachukua hatua kadhaa kuficha uhalisia wao. Usingeweza kudhani kama ndani ya gari hilo lililokuwa limechafuka matope kuna mtu mkubwa kama Samweli, lakini pia usingeweza kudhani kama wale wanaume wawili waliokuwa wanamtazama na kumsikiliza Samweli, walikuwa ni makachero. Sio tu kwamba walivalia kiraia, hapana. Walikuwa pia wachafu kama wengi waishio maeneo hayo.

      Kuna mahali wamepahisi panaweza pakawa kitovu cha kikundi hicho. Wanaume hao wawili baada ya kuketi kwa siri eneo hilo huku wakiwa wanapeleleza kwa macho ya upande, waligundua mahali hapo pa siri. Ni mahali ambapo si watu wote huingia, isipokuwa ijumaa tu kwa ajili ya sala; ni mahali palipojitenga mbali kidogo na makazi ya watu; ni mahali ambapo nje yake kuna wanaume wawili wanaopalinda, na wanaume hao hubadilishwa kila baada ya siku moja na kuja wapya.

      Hakuna mwenye taarifa kamili kuna nini ndani ya eneo hilo, na kabla ya kuchukua hatua yoyote dhidi ya eneo hilo ndipo makachero hao waliamua kuonana na mkuu wao awapatie amri.

      “Ni lazima kwanza tuwe na uhakika kabla ya kuchukua hatua,” alisema Samweli kwa msisitizo. “Leo ni ijumaa na muda si mrefu …” akatazama saa yake mkononi, “muda si mrefu wataanza sala. Kwahiyo basi mtumie hiyo fursa kusali humo na mpekenyue kuna nini.”

      Hiyo ikawa imeeleweka. Wanaume hao wawili walishuka toka kwenye gari, Samweli akaondoka. Walikuwa mbali na mji kwa sababu za usalama, kwahiyo kurudi kwenye makazi walilazimika kutembea kama lisaa limoja.

      Walimaliza lisaa hilo wakaingia ndani ya mji, lakini kila mtu kwa upande wake. Walifikia kwenye makazi yao ya kuzugia, kila mmoja akiwa na yake, kisha wakajiandaa kwa ajili ya kwenda msikitini. Walivalia kanzu, mmoja yake ikiwa nyeusi na mwingine ikiwa nyeupe.

      Adhana ililia ikawakuta wakiwa njiani kwenda msikitini. Walifika mlangoni wakakaguliwa kama wana silaha, ilipothibitika wapo safi, wakaruhusiwa kuzama ndani kama wengineo. Waliswali ndani ya msikiti huo lakini akili yao ikiwa haipo ibadani. Walikuwa wanaperuzi kutazamataza mazingira katika namna ya siri.

      Kulikuwa kuna holi kubwa la kuswalia walipokuwa wamejazana watu kama hamsini na kitu hivi, wote walikuwa wanaume. Wanawake walikuwa kwa upande wa pili huko, nyuma ya mwongoza ibada aliyekuwa upande wa kaskazini mwa holi. Upande wa kusini mwa holi kulikuwa kuna milango miwili iliyokuwa imefungwa. Zaidi ya hapo hakukuwa na lolote la kukufanya uwaze kuna nini mule ndani.

      Sasa kwanini kulikuwa kunalindwa? Tena na watu wabadilishwao kila baada ya muda fulani?

      Maswali hayo yaliwafanya makachero wale wawili waendeleze macho yao ya upekuzi. Baadae wakati ibada yaelekea ukingoni, kachero mmoja akagundua kitu pale alipokuwa amekanyaga. Palikuwa pamefunikwa na zulia jekundu na hivyo basi ukadhania ni sakafu, ila kachero huyo alipopakanyaga mara mbili na kisigino chake aligundua chini ya hapo apakanyagapo pana uwazi. Huweza ikawa ni handaki!

      Alijivunga na hakufanya kitu mpaka ibada yakwisha. Akiongozana na mwenzake, walijipanga katika mstari wa wanaotoka ndani, lakini walipofika mlangoni wakasimamishwa na wanaume wanne waliokuwepo mlangoni. Walikuwa na nyuso za kughafirika. Macho yao yalikuwa makali ambayo yangekufanya uhofie. Mmoja alikuwa ana asili ya kiarabu, wenzake watatu wakiwa weusi kama mie na wewe.

      Kwa ishara yule mwarabu akaonyesha uelekeo wa kusini. Mkono wake wa kuume ulikuwa umeshikilia bunduki kubwa iliyokuwa ndani ya kanzu. Kwa kuhofia usalama wao, makachero wale wawili wakatii amri. Walisindikizwa na wanaume hao wanne mpaka ndani ya chumba kimoja upande wa kusini mwa holi.

      Mlango ulifungwa tusijue nini kilichoendelea humo ndani. Ila baada ya kama robo saa, damu nzito ilichuruzika ikitokea chini ya mlango.



      http://pseudepigraphas.blogspot.com/

      ***





      Si punde nyingi taarifa inamfikia Al Saed kwa njia ya barua pepe. Kwa muda huo hakuwa na habari yoyote na aidha alikuwa anangojea habari njema ya kuteketezwa kwa ‘kijikundi’ cha AMAA, wapumbavu waliokuwa wameanza kumchezea sharubu.







      Alikuwa amekaa kwenye uwanda wa nyumba yake, ikulu, macho yake ndani ya miwani yakiwa yanatembelea baadhi ya mikataba iliyokuwa mbele yake, mikataba iliyokuwa inahusisha nyanja mbalimbali za kimaendeleo mathalani uvuvi, ukulima na madini. Macho yake yalikuwa yamezama ndani ya makaratasini akiwa amebeba tahadhari kubwa. Lakini ghafla anashikwa begani na kutibuliwa utulivu huo.

      “Kuna ujumbe wako, mkuu.” Alikuwa ni mtumishi wake aliyevalia suti nyeusi akitamka.

      “Kutoka kwa nani?” aliuliza Al Saed akiendelea na kazi yake ya kupekua mikataba.

      “Mr X,” akajibu mtumishi.

      Moyo wa Al Saed ukapasuka. Alivua miwani yake akamtazama mtumishiwe.

      “Una uhakika?”

      Uso wake ulitambaliwa na puzo la shaka. Hata kabla hajajibiwa alionekana kupata jibu la swali alilouliza.

      “Ndio, mkuu. Umeingia sasa hivi!”

      Al Saed alipandisha kichwa chake juu kabla hajamruhusu mtumishi wake aende zake. Alibakia kitini kwa muda kidogo akitafakari na kubashiri nini ambalo Mr. X atakuwa amelituma. Kwa namna moja kubwa aliona si alama njema kupokea ujumbe toka kwa Mr. X kwanza kabla ya ujumbe toka kwa Samweli.

      Alishusha pumzi ndefu akaenda ndani. Alimkuta mtumishi wake yupo karibu na tarakilishi yake mpakato, akaivuta na kutazama. Loh! Hakukuta maneno yoyote bali picha; picha za kutisha na kusisimua; picha za vichwa vitatu visivyo na viwiliwili!

      Kama vile aliyemtumia picha hizo alijua ya kwamba Al Saed yupo hewani, mara ujumbe mfupi unaingia. Al Saed bado alikuwa kwenye pumbazo la kujiuliza zile picha azitazamazo ni za nani na kwanini ametumiwa. Alishtushwa na ujumbe huo, haraka akarusha macho yake kuusoma:

      “Hiyo ni salamu kwako kafiri, usithubutu kufanya jambo lolote la kipumbavu.”

      Al Saed alidadavua ujumbe huo kwa dakika moja, haraka akampigia simu Samweli na kumjuza. Habari hiyo ikapokelewa kwa mshangao; Samweli hakutegemea kama ingalikuwa rahisi kwa makachero wake anaowaamini kumalizwa namna hiyo. Ilimlazimu sasa kuchukulia jambo hilo kwa namna tofauti; kwa namna nzito na kwa umakini zaidi.

      Hawakuongea sana, simu ikakatwa. Al Saed aliendelea kutazama picha alizotumiwa kwa takribani dakika tatu. Kila alipojaribu kutuma ujumbe wa kumjibu Mr. X, ujumbe haukwenda. Uligoma na kumtaka aweke kwanza anwani ndipo apate kutuma. Al Saed akaishia kughafirika na kutoka ndani.

      Miwani sasa ilibidi ibadilishwe, pasi na shaka. Jambo lilikuwa kubwa kuliko walivyodhania, lakini pengine bado lilikuwa kubwa kuliko ambavyo bado wanadhania.

      Wafuasi wa AMAA, si kwamba walikuwepo ndani ya kile kijiji kidogo tu, walikuwa wametapakaa maeneo yote ya karibu na eneo hilo wakiwa wamejihami kwa silaha nzito lakini pia wakiwa wamejiweka katika mazingira ya kujificha vya kutosha kiasi cha kutoonekana kwa wepesi.

      Kijiji kizima kilikuwa kina mahesabu kamili ya wanamgambo hao wa kikundi cha AMAA. Hiyo ndiyo ilikuwa ngome yao na hivyo basi kila namna iendeleayo humo walikuwa wanaifahamu. Kila mwanakijiji alikuwa ni mhusika wa kikundi hicho aidha kwa njia moto ama vuguvugu. Kila mgeni aliyeingia humo alitazamwa kwa ukaribu akifuatiliwa nyendo haswa.

      Shaka kwa makachero wawili wa Samweli lilikuwa ni la kawaida hapo awali. Hata wenyeji wao hawakuwa wameng’amua lolote la kugutusha. Ila pale gari la Samweli lilipotua maeneo hayo, ndipo mambo yakaanza kuwa uchi.

      Walifwata nini ndani ya lile gari? Kwanini gari halikuja ndani ya kijiji? Nani yupo ndani ya gari? Hapo ukakasi ukaanza. Japokuwa makachero hao na mkuu wao, bwana Samweli, walidhani wapo wenyewe baada ya kukiacha kijiji kilomita kadhaa, ukweli ni kwamba kulikuwa kuna watu watatu ambao walikuwa wanatazama gari hilo na darubini kali.

      Lakini kama kuna kosa kubwa ambalo makachero hao walilifanya basi ni kwenda msikitini siku hiyo hiyo baada ya kuonana na mkuu wao. Mbona siku zote hawakwenda na ingali walikuwemo ndani ya kijiji? Mosi. Pili, walitolea wapi kanzu mpya wakati hali yao ya kimaisha ilionekana ni duni? Walijichimbia kaburi. Jicho la karibu lililokuwa linawatazama likageuka kuwa upanga uliokula vichwa vyao.



      ***



      Agizo la Raisi ni amri. Japokuwa kishingo upande, Kone alijiandaa kwenda Sierra Leone kutimiza alichotumwa. Yeye ni nani abishane na Raisi?

      Macho yake yalikuwa yamevimba. Uso wake ulikuwa na uchovu. Ulikuwa ni muda wa jioni akiwa tayari ameshakata tiketi ya ndege ya kumtwaa masaa manne mbele. Alioga kisha akachukua mashati mawili aliyoyatupia kwenye gari. Alijiveka viatu vyeusi vya ngozi vilivyokuwa vinang’aa, akamwita mlinzi na kutoka naye garini.

      Hawakuongea neno lolote mpaka pale walipokaribia uwanja wa ndege. Kone alikuwa mwingi wa mawazo. Alisonya kwanza kabla hajasema kwa uchovu:

      “Nadhani unakumbuka niliyokwambia.”

      Mlinzi akatikisa kichwa chake kukubali.

      “Ndio, kiongozi. Nakumbuka.”

      Kukawa kimya tena mpaka wanaingia eneo la uwanja wa ndege.

      “Nakuamini,” alisema Kone. “Natumai hautoniangusha.”

      “Sitakuangusha kiongozi wangu.” Mlinzi akasema kwa kujiamini.

      Kone alivuta begi fulani dogo toka viti vya nyuma, akalipakia mashati yale mawili kisha akashuka akienda ndani ya uwanja. Mlinzi alijisogeza kwenye kiti cha dereva, akatia moto gari apate kutimka. Alirudisha nyuma gari, ila kabla hajaondoka alisikia gari likipigwa kwa nyuma. Alitazama kwa kutumia vioo vya pembeni, akamwona Kone!

      “Hakuna safari!” Kone aliwaka akiwa dirishani mwa gari. “Safari zote za kwenda Sierra Leone zimesitishwa mpaka pale taarifa itakapotolewa.”

      Mlinzi akaachama kwa mshangao.

      “Kumbe taarifa ilitolewa masaa kadhaa hapo nyuma, sikutazama simu!”

      Kone alitabasamu. Mlinzi alikuwa anamtazama mwanaume huyo kwa macho ya duwazo, na kwa namna fulani alihisi Kone anaweza akawa amechanganyikiwa.

      “Kwanini safari zimesitishwa?” Mlinzi aliuliza.

      “Ni kwasababu za kidiplomasia. Hakuna mahusiano mazuri kati ya Sierra Leone na Guinea kwa sasa. Hawatutaki nchini mwao!”

      Gari lilitoka uwanja wa ndege mlinzi akiendesha. Kone alimpigia simu Raisi akamjulisha kuhusu jambo la Sierra Leone. Raisi kwa utulivu akaagiza kwa sauti yake nzito:

      “Ni lazima leo uende Sierra Leone kwa namna yoyote ile, Kone.”

      Uso wa Kone ukawa mweusi.

      Raisi alikata simu. Baada ya robo saa akapiga tena kumpa maagizo Kone. Alimtaka aelekee mashariki kusini kuukuta mpaka uwatenganishao na Sierra Leone. Huko atakuta usafiri utakaomwingiza ndani ya nchi hiyo kimagendo.

      Haikujalisha Kone alikuwa amekwazika namna gani, gari liligeuza mwelekeo kutii amri ya Raisi. Baada ya masaa matano wakawa wamefika panapotakiwa. Kone alikuta gari aina ya van rangi ya bluu iliyokoza. Lilikuwa limechoka mno na lilikuwa linakaribia kujaza watu, hohehahe kwa hali, lipate kutimka.

      Ndani ya gari kulikuwa kuna wanyama mathalani kuku, mbuzi na ndama. Lakini pia lilikuwa limejaa joto na uvundo. Sura za watu waliomo humo zilikuwa zinarandana kwa ukata na kuchakaa.

      Kabla ya Kone kupanda humo, alimuuliza kondakta:

      “Kuna usalama wa kufika Sierra Leone?”

      Kondakta alimtazama kwa mshangao.

      “Ndio mara yako ya kwanza kwenda Sierra?”

      “Hapana,” akajibu Kone. “Ila ndiyo mara ya kwanza kutumia usafiri huu.”

      Kondakta akatabasamu.

      “Usijali, usalama upo. Ila bila shaka utatusaidia endapo tukikamatwa na wanajeshi.” Alisema akimtazama Kone. Bila shaka alimwona ni wa tofauti.

      “Kivipi?”

      “Usijali, ni kuwahonga tu. Ukiwapatia kitu kidogo basi wanaturuhusu. Huwa tunafanya hivyo mara kwa mara endapo wakishikwa na njaa.”

      Kone alitikisa kichwa chake kwa masikitiko. Alitazama lile gari analoeleka kupanda, akajikuta akitokwa jasho. Aliagana na Mlinzi wake kisha akajitweka ndani ya gari hilo mbanano, na punde safari ikaanza.

      Ni umbali mfupi tu tokea pale safari ilipoanzia mpaka ndani ya Sierra Leone, ila kwa mujibu wa gari lile ambalo lilikuwa linasimama na kubustiwa, ama kutiwa maji ndio lipate kwenda, wakatumia masaa manne kuingia.

      Ilikuwa ni usiku sasa. Kone alilazimika kutafuta mahali pa kulala. Alikosa kabisa sehemu nzuri akaishia kulala kwenye nyumba fulani iliyochoka mno, akipewa hifadhi na mzee mmoja mkarimu. Alipata chakula hapo na kukabidhiwa mkeka autumie kama kitanda. Mazingira hayo yalimwia vigumu lakini hakuwa na namna zaidi ya kukabiliana nayo.

      Mwenyeji wake alimwambia mahali hapo huwa panatembelewa mara kwa mara na wanajeshi kwasababu ya kukaa karibu na mpaka, hivyo basi asiwe mtembezi. Akatii.

      Alimpigia simu Rose, akawa hapatikani. Wakati akiendelea bado kumtafuta mwanamke huyo alijikuta akipitiwa na usingizi mzito kutokana na uchovu mkali. Alikuja kuamka saa kumi na mbili asubuhi ambapo aliaga na kufanya mpango wa kuitafuta Freetown.

      Akiwa njiani alimpigia simu Mlinzi, simu ikaita mara tatu pasipo kupokelewa. Aliachana na hilo zoezi lakini haikupita muda mrefu, simu ya Rose ikaingia. Alipokea na kumtaka mwanamke huyo waonane ndani ya jiji la Freetown baada ya masaa kadhaa, Rose akaridhia.

      Mwanamke huyo alikuwa ndani ya hoteli kubwa wakila raha na Talib. Ilimpasa aende chooni kuwasiliana na Kone kwasababu za usalama. Alimwomba Talib muda wa kwenda kupumzika nyumbani kwake, Talib pasipo na kinyongo akamruhusu. Alijiweka kwenye gari lake, akiendesha yeye mwenyewe, akaenda mpaka nyumbani kwake.

      Alioga na kujivesha nguo maridadi kabla tena hajatoka nyumbani kwake, na mazingira yasiyomjuza, akaelekea mahali fulani ufukweni mwa bahari. Miwani yake kubwa ya macho na nywele nyingi za bandia zilimfanya asijulikane kama ni katibu mkuu wa nchi, bali mwanamke fulani aliye kwenye starehe zake.

      Ilikuwa imebakia kama nusu saa tu, Kone atinge ndani ya Freetown. Alikuwa amesinzia kwenye kiti cha basi akiwa ameegemea kioo cha dirisha. Alikuwa amechoka, ungeweza kumwona kwa macho tu. Mdomo wake ulikuwa umeachama akikoroma kwa mbali.

      Simu yake iliita mara nne, hakusikia. Alikuja kugundua hilo aliposhuka toka kwenye basi baada ya kushtuliwa na kondakta kuwa basi limefika mwisho. Kioo cha simu yake kilimjuza Mlinzi alimtafuta mara zote hizo. Pasipo kujivunga, akaamua kumpigia.

      “Amekuja leo kumjulia hali,” Alisema Mlinzi.

      “Lile lile gari?”

      “Ndio, amekuja leo asubuhi na mapema, sijui amejuaje kama shemeji yupo hapa.”

      “Umemfuatilia?”

      “Ndio! Nimemfuatilia mpaka nyumba aliyoingia.”

      “Safi sana. Umefanya kazi nzuri!”

      “Lakini kiongozi kuna jambo kidogo.”

      “Niambie.”

      “Kwenye nyumba ambayo gari hilo limeingia, kuna ulinzi mkali mno. Ni ngumu hata kusogea karibu; inaonekana huyu jamaa ni mtu mzito serikalini.”

      Kone akanyamaza kwa muda. Alijaribu kuvuta picha ya huyo mtu kichwani kumbukumbu zake zikagoma kabisa kuunga mkono hoja kwamba anamjua. Ni mtu gani mzito kwenye serikali hii ya Guinea asipate kumjua? Aliwaza.



      ***

      Liberia: ndani ya chumba chenye mwanga hafifu.

      Walikuwemo watu watatu ndani ya chumba kimoja msikitini. Nyuso zao hazikuwa zinaonekana vema kutokana na uhafifu wa mwanga. Wawili walikuwa wamevalia kanzu nyeusi na mmoja pekee ndiye alivalia kanzu nyeupe. Walikuwa wameketi chini wakitengeneza umbo la pembe tatu.

      Kulikuwa ni kimya usidhani kama kuna watu.

      “Nadhani maelezo yote umeshayapata,” alisema mwanaume mmoja ndani ya kanzu nyeusi. Sauti yake ilikuwa nzito na ya kukwaruza. “Wewe ndiye umeteuliwa kufanya sadaka hii, utasaidiana na mwenzako hapo. Ni muda sasa wa dunia kujua uwepo wetu rasmi.”

      Baada ya kusema hayo, mwanaume huyo alipeleka mkono wake wa kuume upande wa kushoto nyuma kwake, akavuta begi fulani kubwa. Alilisogeza karibu na yule pekee aliyevaa kanzu nyeupe akisema:

      “Kila kitu mnachohitaji kipo humo. Kila kitu mnachohitaji kwenye kufanya kazi yako hii takatifu.”

      Pasipo kuhakikisha kama yasemwayo ni kweli, yule mwanaume aliyevaa kanzu nyeupe alilitwaa begi akatikisa kichwa chake.

      “Tutafanikiwa kama vile Mungu apendavyo.”

      Wenzake wakatikisa kichwa na kumwekea viganja kwenye bega lake la kulia.

      Asubuhi na mapema, gari dogo jekundu Toyota Starlet linatoka kijijini hapo likiwa limebebelea wanaume wawili. Wote wamevalia kiraia. Macho yao makubwa yanaangaza na nyuso zao zimejawa tahadhari.

      Kwa mwendokasi wa wastani gari hilo lilitembea. Mpaka kufikia karibu na jioni, walikuwa tayari wameingia ndani ya jiji la Monrovia. Walikodisha chumba cha malipo nafuu wapate kumpuzikia hapo. Walikula chakula cha kawaida na kuswali kabla ya kulala.

      Asubuhi ya mapema, waliamka wakaswali. Mmoja, mweusi kuliko mwenzake, alivua nguo zake akibakiwa na nguo ya ndani pekee, mwenzake akaanza kumfunga ‘kikoti’ cheusi alichokitoa ndani ya begi, kisha akamfunga na mkanda mnene mweusi kiunoni. Baada ya hapo akahakikisha kama vitu hivyo vimekaa vema. Aliporidhika, alimvesha mwenzake kanzu yake na kumkabidhi rimoti ndogo.

      Walitazamana wakawekeana viganja kwenye mabega yao ya kulia na kutikisa vichwa vyao. Kisha wakatoka ndani kuendea gari.







      Kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2008, jiji la Monrovia lilikuwa lina watu takribani milioni moja na kumi elfu mia tisa sabini. Ni jiji lenye watu wengi zaidi nchini humo likiwa na pilikapilika za hapa na pale za kibiashara. Lakini biashara hizi zikiwa nyingi ni za umachinga watu wakitandaza bidhaa chini na kungojea wateja.

      Ndani ya jiji hilo kuna masoko makubwa mawili ambazo ndaniye ndimo watu wa nchi hiyo hupata bidhaa nyingi toka nje ya nchi hiyo, ama twaweza kuziita bidhaa za kimagharibi. Watu hujazana humo haswa kipindi cha mwisho wa juma.

      Huu muda sasa ulikuwa ni mwisho wa juma na watu walikuwa wamejazana vya kutosha ndani ya masoko hayo mawili kama ilivyo ada wakinunua bidhaa mbalimbali. Nje ya soko mojawapo kati ya hayo mawili, lilisimama gari lililowabebelea wanaume wale wawili waliotoka kwenye nyumba ya wageni.

      Mwanaume yule aliyejikoki kwa kujazwa mambo lukuki ndani ya kanzu, alitoka ndani ya gari hilo na kuendea ndani ya soko. Mwendo wake ulikuwa wa taratibu na uso wake haukuonyesha shaka lolote.

      Mwenzake alimtazama akiyoyoma ndani ya soko, kisha akawasha gari na kutoka eneo la karibu na soko hilo. Alikwenda umbali wa kama nusu kilomita kisha akalituamisha gari hapo na kurusha macho yake kutazama soko lile lililommeza mwenzake.

      Baada ya dakika kama tano, mtikisiko mkubwa wa ardhi ukavuma ukiambatana na sauti kubwa ya mlipuko. Soko aliloingia yule mwanaume lilishika moto mkubwa na sauti za yowe zikateka jiji! Ilikuwa mvurugano watu waliosalimika wakikimbia na kukanyagana. Wengine wakivuja damu nyingi maeneo mbalimbali ya miili yao.

      Mwanaume yule ndani ya gari alitabasamu kabla hajakanyaga pedeli za mafuta kuondoka eneo hilo.

      “Tayari, yamekwisha,” aliwataarifu wenzake kwa kutumia simu.









      ***









      Haraka vyombo vya habari vya kitaifa na kimataifa vikarusha tukio hilo la mlipuko wa soko kubwa ndani ya jiji la Monrovia, Liberia. Watu wapatao themanini na tano waliripotiwa kufia papo hapo, huku wengine kama arobaini na kitu wakiwa ni majeruhi.

      Damu zilitapakaa ndani ya soko hilo ambalo liligeuzwa sehemu ya maombolezo ndani ya muda mfupi mno!

      AL Saed aliyekuwa anatazama tukio hilo runingani alijikuta anasinyaa moyo, macho yake yakimtoka pima. Kama vile tamthilia utamuni alipata kutazama. Mkono wake wa kuume uliunda ngumi na mdomo wake ukasaga meno. Alijiona yumo matatani, na hatua ya haraka inabidi ichukuliwe kuzuia upumbavu huo.

      Hakuna wengine zaidi ya AMAA! Aling’aka. Alishangazwa ni kwa namna gani watu hao wanavyolazimisha taifa kugeuzwa kuwa la kidini kwa kuua watu wasio na hatia. Ni uslamu gani huo wanaousimamia? Hapana, hawa watakuwa wana ajenda ya siri; watakuwa wana ajenda binafsi mbali ya pumbazo la dini!

      Upesi Al Saed alimpigia simu Samweli na kumtaka aje ikulu. Ndani ya muda mfupi, yeye na Samweli wakawa wamo kwenye chumba cha majadiliano wakiteta mustakabali wa usalama wa nchi.

      “Kama tukiendelea kutochukua hatua, watatumaliza,” alisema Samweli akiwa ametoa macho ya ukali.

      Mwanaume huyo ahusikaye na usalama hakuona tena kama kuna haja ya kujiuliza mara mbilimbili kuhusu kuvamia na kuharibu kijiji kizima kinachotuhumiwa kufadhili kikundi cha wanamgambo wa AMAA. Jambo hili kwake lilikuwa jema lakini kwa Al Saed bado lilikuwa la ukakasi.

      “Hakuna njia ya kuwamaliza hawa wanamgambo pasipo kuwaua hata na wananchi wasio na hatia kijijini hapo?”

      “Mkuu ni bora tukaua watu hamsini kwa ajili ya kuokoa taifa zima,” alishauri Samweli. “Endapo kama tukifiria hivyo basi ni wazi hakuna siku tutakuja kuchukua maamuzi. Kijiji kile hakiingiliki kwa urahisi. Muda haungoji na watazidi kukua zaidi.”

      “Kwahiyo unashauri tuwaangamize kwa njia gani?”

      “Tutume jeshi likawatawanyishe.”

      “Mawazo yako ni mema, ila yasitawaliwe na papara. Hatujajua wamejipangaje hawa watu haswa baada ya kufanya tukio hili kubwa. Inabidi kutazama nyendo zako vema kabla ya kuzamisha kichwa.”

      Maongezi hayo yalidumu kwa muda wa nusu saa: wakakubaliana Samweli aendeshe operesheni hiyo ‘tokomeza’ baada ya siku mbili za upembuzi yakinifu. Samweli akamuaga kiongozi wake kisha akaenda kukutana na viongozi wa juu wa jeshi kuwajulisha kuhusu mpango huo kabambe. Alitaka vikosi viwili vya jeshi viandaliwe na kuwekwa bayana kushambulia muda wowote. Wakuu wa jeshi wakapokea taarifa hizo na kuzivalia njuga.

      Lakini juu ya mpango huo kulikuwa kuna msisitizo wa siri na umakini mkubwa kwani kushindwa kwa mpango huo kutasababisha hali iwe mbaya zaidi. Halikuwa jaribio bali tendo litakalorudisha nchi kwenye mikono ‘salama’ tena.

      Lakini kauli kumbuzi ya Mr. X bado ilikuwa inarandaranda ndani ya kichwa cha Al Saed. Kwa namna moja ilikuwa inamuogopesha na kumfanya afikirie jambo hilo mbele yake mara nne nne.

      “Hiyo ni salamu kwako kafiri, usithubutu kufanya jambo lolote la kipumbavu.”

      Jambo lake hili la ‘kipumbavu’ litafanikiwa? Lazima lifanikiwe! Alisema na moyo. Alimpigia simu Samweli akamwambia hataki taarifa yoyote ya kushindwa toka kwenye zoezi hilo.





      http://pseudepigraphas.blogspot.com/



      ***

      ***









      Televisheni bado ziliendelea kuonyesha maswahibu yaliyotokea kwenye soko kubwa huko Monrovia. Saa hii, wakati wa jioni, Rose na Kone walikuwa wakitazama tukio hilo wakiwa kwenye eneo kubwa la wazi ndani ya hoteli kubwa ya kifahari.

      Rose alikuwa amevalia nywele nyingi za bandia lakini pia pasipo kusahau miwani kubwa iliyotwaa zaidi ya nusu ya uso wake. Kone alikuwa amevalia shati jeupe jepesi alilolichomekea ndani ya suruali yake ya kitambaa rangi ya kahawia.

      Meza yao ndogo lakini imara ilikuwa imebebelea juisi ndani ya glasi kubwa ndefu, huku Rose akiwa ameambatanisha na vitafunwa vyake avipendavyo: sambusa za nyama. Waliketi mbali kidogo na watu wachache ambao walikuwepo eneo hilo. Hata maongezi yao hayakuwa ya kusikika; yalikuwa binafsi.

      “Nafasi ipo tena kubwa sana, Kone,” alisema Rose. “Sema tu tunahitajika kuwa wapole kwa sasa. Hatuwezi tukakurupuka kukwapua ukizingatia muda mchache tuliopo madarakani.”

      Kone alitikisa kichwa chake akanyonya juisi mrijani.

      “Kwahiyo ni kama muda gani utakuwa tayari kutimiza hilo?”

      “Nipe angalau miezi mitatu.”

      “Wasema? – Hapana haiwezekani, Rose!”

      Kone hakuwa radhi kupoteza miezi yote mitatu, kwake huo ulikuwa ni muda mrefu sana maana wamaanisha ni muda wa kutokuwa na familia yake. Hapana! Sasa alikuwa amechoka kuzunguka nchini mwa watu na alikuwa anataka atulie kando na wanawe na hata mkewe aliye hoi.

      Rose hakuwa anayaelewa hayo. Kone alimweleza mwanamke huyo kinaganaga juu ya yale yote anayoyapitia pasipo kumficha jambo. Rose akamwonea huruma sana Kone, lakini pia akashangazwa.

      “Kwanini Raisi anafanya hivyo?”

      Kwa muda wote huo wakati Kone alivyokuwa anaeleza, Rose alikuwa ameacha kufanya kila kitu akitazama uso wa Kone uliokuwa umesinyaa kwa msongo wa mawazo. Kwa kupitia macho ya mwanaume huyo ungelipata kuona ni namna gani moyo wake ulivyoraruriwa: namna gani mwanaume huyo alivyojeruhiwa na hisia.

      “Kone, kuna kitu,” alisema Rose. Uso wake haukuwa na shaka wakati anatamka hayo. “Mi nakushauri uwe makini sana na uweke macho na masikio yako wazi muda wote. Ni lazima kutakuwa na sababu iliyomfanya Raisi akawa hivyo.”

      Waliteta na hilo jambo kwa muda wa kama dakika kumi kabla Rose hajahitimisha kwa kushauri:

      “Kone, rudi nyumbani ukakae na familia yako.” Yalikuwa ni maneno machache mazito. Kone alipoyapokea alivuta pumzi ndefu akanyonya juisi yake kupoza kifua.

      “Sidhani kama ni rahisi kiasi hicho, Rose.”

      Alihofia usalama wake. Kwa namna moja ama nyingine aliona ni bora akafanya vile atakavyo Raisi kwani akikaidi anaweza akajikuta yupo mbali zaidi na familia yake, ama kutoiona tena.

      “Kone, mkeo yupo hospitalini, anakuhitaji sana muda huu. Na watoto wako je? Wataendelea kuwa wapweke mpaka lini ingali wana wazazi?”

      “Natambua yote hayo, lakini unajua mimi ni unyoya tu mbele ya kauli ya Raisi. Anaweza kunipoteza ndani ya sekunde na asiwepo mtu yeyote wa kumuuliza!”

      “Kwani Raisi anakuja nyumbani kwako? – Rudi nyumbani na uniachie mimi hiyo kazi yako, nitaifanya. Sidhani kama ukirudi tu basi Raisi atakuona. Kwani ana macho nchi nzima? …”

      Kabla Rose hajaendelea zaidi simu yake ilimtaarifu anahitajika na Talib kwa kupitia ujumbe mfupi. Alimuaga Kone akimsisitizia afanye yale aliyomwagiza, kisha akaondoka.

      Kone alimsindikiza mwanamke huyo na macho yake yaliyochoka. Alimalizia juisi yake naye akaondoka kwenda mahali alipofikia kwa ajili ya mapumziko.

      Alijitupia kitandani haraka kichwa chake kikatwaliwa na mawazo ya nyumbani kwake: mkewe na watoto. Alitamani kupiga simu kuulizia huko nyumbani lakini akakumbuka alifanya jambo hilo muda si mrefu sana. Alifikiria kuhusu maneno ya Rose na ushauri wake lakini bado nafsi yake ikawa na majibizano; ilikuwa ngumu sana kwake kuamua. Aliwaza na kuwaza mpaka akalala. Alikuja kuamshwa baadae na mlio mkali wa simu. Alikuwa ni Mlinzi anamtafuta.

      Kabla hajapokea alitazama saa yake mkononi, akaona ni majira ya saa sita na dakika ishirini na tatu usiku.

      “Kiongozi,” sauti ya Mlinzi ilifunua mjadala. “Samahani kwa usumbufu, kuna jambo nataka nikutaarifu.”

      Macho ya Kone yalikaa tenge akingojea ujumbe huo anaotaka kupewa.

      “Yule jamaa amekuja leo hospitali, na amemwamishia shemeji hospitali nyingine!”

      Moyo wa Kone ukapiga tuff! Alitaka aufungue mdomo kwa pupa, ila akajikuta ananyamaza baada ya kusikia sauti ya Mlinzi ikiendelea.

      “Leo hii jioni alikuja akiongozana na polisi wanne, sikuweza kufanya kitu kabisa. Niliwauliza polisi wale wanampeleka wapi shemeji lakini hawakusema kitu. Hata nilipotaka kuongea na mwanaume huyo, nilizuiliwa na kukatazwa kujongea karibu kabisa!”

      Betri lilikata nguvu kwenye simu ya Mlinzi, simu ikakata kwa kuzima. Kone aliwehuka na hakupata usingizi usiku wote huo. Ilipofika saa kumi na moja kasoro alipaki vitu vyake vyote akaenda kwenye kituo kikubwa cha mabasi, alikata tiketi na kujiweka kitini akiona muda hauendi kabisa!

      Alimtumia ujumbe Rose:

      “Nipo njiani narudi nyumbani.”











      ***









      Wakati ujumbe wa Kone unaingia kwenye simu ya Rose, Talib ndiye alikuwa ameshikilia simu hiyo akiperuzi mtandaoni. Rose alikuwa bafuni anaoga.

      Ilikuwa ni ndani ya Ikulu kwenye kitanda kikubwa chenye shuka zito jeupe na mito ya kumwaga. Chumba kilichopendeza kwa samani za haja na kuvutia. Sina haja ya kueleza sana kuhusu mahala hapa maana tayari nomino ‘Ikulu’ ilishatangulia.

      Talib alivutiwa kusoma ujumbe huo kwa msukumo wa wivu. Jina la aliyetuma lilikuwa limetunzwa simuni: ‘Kone-Bro’. Aliufungua ujumbe huo akausoma kisha akamngojea Rose aje kumfafanulia.

      Rose alitoka bafuni akiwa anajikausha nywele zake ndefu. Mwendo wake ulikuwa wa madaha na alienda kuketi kitandani kumkuta Talib.

      “So hauendi tena?” Rose aliuliza.

      Tokea majira ya asubuhi Talib alikuwa ana miadi ya kukutana na chama cha wafanyakazi ambao walikuwa wanataka kumwelezea na kumlalamikiia kuhusu madai yao sugu ambayo yamekuwa yakipuuziwa na kupigwa danadana muda nenda muda rudi, tokea utawala ule nyuma ya Kessy.

      Tokea muda huo wa asubuhi, wanachama hao walikuwa kwenye uwanja mkubwa wa mkutano wakimsubiria kiongozi huyo ambaye alikuwa na Rose Ikulu akiwa hana habari yoyote.

      “Siendi popote,” alijibu Talib akimwonyeshea Rose simu. “Huyu nani?”

      Rose alishtuka lakini alifanikiwa kutomwonyesha Talib chochote. Aliigiza tabasamu akajibu akiendelea kufuta nywele zake.

      “Jamani si unaona nimemsevu Bro. acha wivu mpenzi!”

      “Hukunambia kama una kaka.”

      “Yah! Sio kaka wa tumbo moja, hapana. Ni mtoto wa baba mkubwa. Sasa mpenzi n’tatambulisha familia yote?”

      “Ulionana naye, leo?”

      “Ndio. Nilimwacha nyumbani wakati nakuja huku.”

      Waliachana na hilo jambo wakazama kwenye ulimwengu wa mahaba kwa kukumbatiana na kupeana mabusu motomoto. Kama watoto wakavutana na kuchezea mito. Walikumbushiana utoto ‘walioumisi’ na muda si mrefu hamu zikajaza bongo zao wakaanza kunyonyana ndimi wakipapasana maungo.

      Rose alikuwa anatoa miguno ya haja. Uso wake ulionyesha kweli amezama, lakini hakuna anayejua kama kweli kichwani alikuwa hivyo ama alikuwa anaigiza. Hakuna mtu anayemjua vema Rose isipokuwa yeye mwenyewe. Ni muumba wake pekee ndiye anaweza kuhangaika na kichwa cha mwanamke huyo.

      Wakiwa humo dimbwini mwa mahaba, mlango wa chumba hicho unagongwa taratibu mara tatu, hakuna anayesikia. Mlango unagongwa tena kwa msisitizo, Talib na Rose wanasikia sasa na kusitisha zoezi lao. Talib alikunja sura akitazama mlangoni.

      “Nani?” Alipaza sauti.

      “Nenda kamsikilize mpenzi.” Rose akashauri.

      Talib alijifunika shuka akaenda mlangoni. Alimkuta mwanajeshi mwenye zamu ya kumlinda akiwa amesimama kwa ukakamavu.

      “Mheshimiwa, kuna tatizo.”

      Talib akasonya.

      “Tatizo gani?”

      “Tatizo kubwa, mheshimwa. Ni bora ukaenda kujionea mwenyewe.”







      Talib alirejea chumbani akajivesha nguo nyepesi kabla ya kutoka ndani na kwenda moja kwa moja kwenye sebule ya ikulu. Mlinzi wake aliwasha runinga akamtaka mkuu wake atazame yaliyokuwa yanajiri kwenye chaneli ya taifa.



      Maelfu ya watu walikuwa wamejazana mitaani wakiwa wamebebelea mabango yenye ujumbe mkali dhidi ya Talib na utawala wake. Maelfu hayo ya watu walikuwa ni wafanyakazi waliokuwa wanadai malimbikizo ya pesa zao tokea miaka na miaka wakiwa sasa wamepoteza matumaini ya pesa hizo baada ya mapuuzo ya Talib.



      Mitaa ilitapika; wafanyakazi hawakuwa peke yao bali pia walisaidiwa na wananchi wengine ambao nao waliona haja ya kufanya hivyo kwasababu ya hali ngumu ya kiuchumi iliyowaloweza kwenye umasikini uliokithiri. Kutokana na maandamano hayo, maduka yakafungwa na shughuli za uzalishaji zikasimama kwa muda.



      ‘TUNATAKA HAKI YETU!’ bango mojawapo lilisomeka hivyo, ‘MATUMBO YANATAKA CHAKULA NA SI SIMULIZI’ ‘POCHI YA SERIKALI NI YA WOTE SI YA WACHACHE’. Hayo yalikuwa baadhi tu ya maneno yaliyopachikwa kwenye mabango yaliyobebelewa na wananchi waliofurika mtaani. Mabango mengine hayakuwa na maneno bali michoro na katuni za Talib akiwa anafanya visa mbalimbali.



      Sauti ilikuwa moja tu, tunataka haki yetu! Watu wote hao walikuwa wanapaza sauti hiyo kwa kuimba. Safari yao ilikuwa ni kuelekea kwenye majengo ya wizara husika wakiapa kutotoka hapo mpaka wajue hatima yao.



      Talib alisaga meno yake akitazama habari hiyo yote iliyokuwa inarushwa mubashara. Alihisi kifua chake kimepata moto na wafanyakazi wanaelekea sasa kumpanda kichwani. Haraka aliwasiliana na waziri wa usalama na ulinzi, akamuuliza:



      “Umepanga kufanya nini mpaka muda huu upo kimya?” Alifoka.

      “Mkuu, naona wapo wengi sana. Nimeona niwaache tu kwani hawana madhara yoyote.”

      “Hawana madhara!” Alitahamaki. “Wanavyonitusi na kunidhihaki unaona sawa?”

      “Hapana mku …”

      “Watoe mtaani mara moja, warudi majumbani mwao! Nadhani unajua namaanisha nini!”



      Baada ya agizo hilo simu ikakatwa kisha Talib akaketi akiendelea kutazama runinga. Sasa alikuwa anangojea kuona utekelezaji wa agizo lake ndani ya muda mchache mbeleni.



      Rose alikuja sebuleni akiwa amevalia gauni la kulalia, akaketi pembeni ya Talib. Macho yake yalitekwa na taarifa ya maandamano iliyokuwa inaonyeshwa. Wakati akitazama taarifa hiyo, alimuuliza Talib juu ya nini kinasibu huko kwenye mitaa ya Freetown. Talib akamjibu kwa jibu jepesi:

      http://pseudepigraphas.blogspot.com/

      “Usijali, muda si mrefu mitaa itakuwa meupe.”



      Jibu hilo lilitosha kabisa kumjuza Rose mambo yatakuwa mabaya kwa wale waandamanaji ndani ya muda mchache. Aliwaonea huruma na alianza kufanya jitihada za kuwakomboa.



      “Talib, sidhani kama njia ya upanga itasaidia.”



      Talib kimya. Macho yake yaliyokuwa mekundu tayari yalikuwa yanatazama runinga.



      Rose alijaribu sana kuongea lakini hakupata msikilizaji. Mwishowe alichoka akaaga anaenda zake. Talib alimsindikiza mpaka kwenye gari, akamwambia maneno machache.



      “Nenda kapumzike; samahani sihitaji ushauri wako kwenye hili.”



      Rose hakusema kitu. Aliingia kwenye gari lake akatoka eneo hilo. Talib alijirudisha ndani akaendelea kutazama runinga. Ndani ya muda mfupi akapata kuona magari ya jeshi yakiwa yanaingia mitaani yakibebelea wanajeshi lukuki wenye silaha nzito. Wanajeshi hao walijitoa magarini wakatapakaa mitaani.



      Talib akatabasamu.



      Mwanajeshi mmoja aliyebebelea kipaza sauti kikubwa, alipaza sauti yake:



      “Tawanyikeni mara moja. Mna dakika tatu tu za kupotea eneo hili!”



      Sauti yake hiyo ilisikika vema lakini ikapuuziwa: hakuna mwandamanaji aliyesikia na kutii agizo. Bado sauti za ‘tunataka haki zetu’ ziliendelea kuvuma na kuwika.



      Tangazo lilirudiwa tena kwa msisitizo. Mara hii wanajeshi walijiandaa wakiwa wamebebelea ngao za kujikinga, virungu na hata bunduki.



      Dakika tatu zilipopita, wanajeshi wakaanza kutimua watu kwa kuwarushia mabomu ya machozi, kuwafyatulia risasi na kuwakung’uta kwa virungu. Watu walikimbia kama wehu kuokoa maisha yao. Kutokana na idadi yao wengine wakaangushwa chini na kukanyagwa vibaya mno.



      Mamia ya watu walijeruhiwa na kuachwa barabarani wakiwa wanavuja damu, wanalia kwa maumivu makali. Wengine walikuwa wamekufa ama kuzirai huku wengine wakiwa ni majeruhi tayari lakini wanaendelea kupewa kipigo kizito kana kwamba wezi ndani ya mitaa ya kariakoo.



      Sasa ilikuwa vita kamili. Waandamanaji nao wasikubali kuonewa, wakaanza kujibizana na wanajeshi kwa kurusha mawe na mabanzi. Wengine walio waovu wakawa wanapasua maduka waibe bidhaa mbalimbali na pesa taslimu. Ilikuwa fujo mno ndani ya jiji.



      Baada ya lisaa limoja kukawa tulivu. Watu hawakuonekana tena mtaani bali baadhi ya magari ya jeshi yakirandaranda. Hospitali za jiji zilikuwa zimefurika mamia ya maiti na miili ya watu. Wengine walio hai na wenye majeraha ya kujikidhi walikuwa ndani ya nyumba zao wakitazama nje kwa kupitia madirishani.



      Talib alikuwa ana furaha sasa, adhma yake ilikuwa imetimia ya kuwatia adabu ‘wakaidi’ kwa kuwaonyesha upande wake wa pili. Ila kwa upande mwingine, taasisi za kimataifa za kutetea haki za binadamu zilianza kubweka zikikemea hali hiyo. Video mbalimbali zilizoonyesha watu wakipigwa kinyama na kuuawa zilisambaa ulimwenguni kote. Huko mitandaoni maneno yakaanza kurushwa na vidole vikanyooshewa Sierra Leone.



      Talib hakujali hata lepe. Alimpigia simu Rose akitaka arejee Ikulu lakini Rose hakupokea simu hiyo, zaidi aliizima asipatikane hewani.



      “Siku yako ipo karibuni,” alisema Rose akiitazama simu yake kana kwamba anaonana na Talib. Uso wake ulikuwa umevimba kwa hasira na hata moyo wake pia.









      ***









      Ilikuwa ni jioni iliyoelemewa na usiku. Kone alikuwa ndani ya gari dogo la magendo lilikuwa linavuka mpaka kwenda Guinea.



      Gari hilo dogo lilikuwa limebananisha watu mno. Wanyama kama mbuzi, ndama na kuku nao walikuwa wamo humo ndani pamoja na binadamu. Kulikuwa kuna joto kali na harufu pia. Japokuwa madirisha yalikuwa wazi lakini hayakusaidia.



      Safari hiyo iliyokuwa inafanyika kwenye barabara mbovu, ikijawa na michanga, mawe na madimbwi ya maji, ilikuwa ina matumaini ya kukamilika ndani ya masaa mawili mbele kwa abiria kuingizwa ndani ya Guinea. Na hiyo ndiyo ilikuwa safari ya mwisho mpaka tena kesho asubuhi na mapema. Kama Kone asingelipata hilo gari basi ingemlazimu avumilie tena mpaka siku inayofwata, jambo ambalo asingeliweza abadani.



      Wakiwa bado hawajamaliza safari yao, ghafla walisimamishwa na wanajeshi wanne waliobebelea bunduki Ak 47. Waliamriwa wote washuke chini na kunyoosha mikono yao juu.



      Abiria wote walitii, wakaacha mifugo tu ndani ya gari.



      “Mnaenda wapi muda huu?” alifoka mwanajeshi mmoja mfupi.

      “Tunaenda msibani, waheshimiwa,” akadakia dereva upesi.

      “Mnatufanya sisi wajinga enh?” alisema mwanajeshi yule mfupi. Alimtazama Kone kwanzia juu mpaka chini, akamuuliza:

      “Wewe ndiye kiongozi wao?”



      Kone alifikiria mara mbili. Alimtazama dereva wa usafiri ule, dereva akamkonyeza kumpa ishara.



      “Hapana, mimi siyo kiongozi wao,” alijibu Kone.

      “Bali?”

      “Ni mwanafamilia tu. Ni mjomba wa marehemu.”

      “Oooh! Pole sana mjomba. Najua unataka sana kuwahi msibani, fanya basi mkono ucheze matairi yaende.”



      Kone alishatambua nini wanajeshi wale wanataka. Alikumbuka maneno ya kondakta wa kwanza kabisa wakati anakuja nchini Sierra Leone kwa kutumia usafiri wa aina ile. Basi akaingiza mkono wake mfukoni na kutoa kiasi fulani cha pesa alichokichambua na vidole vyake, kama laki mbili hivi, akawapatia wanajeshi wale.



      Mwanajeshi yule mfupi alikagua pesa hizo kisha akazitia mfukoni. Alitabasamu akimtazama Kone.



      “Karibu sana na pole kwa msiba.”



      Abiria walirudi ndani ya gari wakaendelea na safari yao. Kwenye majira ya saa nne usiku waliingia Guinea, Kone akipokelewa na mlinzi wake ndani ya gari. Alijiweka ndani ya chombo hicho wakatimua upesi.



      Majira ya nane usiku, Kone na mlinzi wake wakawa wamewasili karibu kabisa na maeneo ambayo Kone aliambiwa na mlinzi wake kwamba ni makazi ya mwanaume aliyekuwa anamchukua mkewe, bi Fatma.



      Kone alikuwa amelala hivyo mlinzi wake akamgutua toka usingizini na kunyooshea kidole jumba hilo.



      “Ndiyo pale.”

      Eneo hilo lilikuwa lina wanajeshi wawili waliobebelea bunduki wakitembeatembea. Palikuwa kimya mno.

      http://pseudepigraphas.blogspot.com/

      Kone alishuka toka garini akasogelea eneo hilo. Haraka wanajeshi wale walitambua ujio wake huo, wakamwamuru asimame haraka na kunyoosha mikono juu akiwa huko huko mbali. Midomo ya silaha zao ilikuwa inamtazama Kone.



      “Unaenda wapi!?” Mwanajeshi mmoja aliuliza. Uso wake ulikuwa umekakamaa kana kwamba kaona gaidi.



      “Samahani kwa usumbufu, nimekuja kumfwata mke wangu!” Kone alipaza sauti yake kavu.



      Wanajeshi walitazamana kwa mshangao kisha wakarudisha nyuso zao kwa Kone.

      “Mkeo? Nani kakwambia mkeo yupo hapa!”

      “Najua yupo hapa. Tafadhali naomba nionane naye, anaitwa Fatma.”



      Wanajeshi hawakutaka kumsikiliza wala kumwelewa, walimfukuza Kone aondoke eneo hilo upesi. Kone alileta ubishi risasi ikapigwa kandokando yake. Alikubali kuondoka lakini akiahidi atarejea. Alijiweka ndani ya gari akaenda nyumbani kwake kupumzika.



      Kesho yake asubuhi kwenye majira ya saa nne alipoamka, aliikuta simuni rekodi tatu za miito toka kwa Raisi, pamoja na ujumbe uliosomeka kwa kuuliza:

      “Nani amekuambia urudi Guinea?”



      Alijikuta anaghafirika, lakini pia akipatwa na maswali. Raisi amejuaje kuhusu ujio wake mapema kiasi hicho?



      Kabla hajajibu ujumbe huo, mlango wa chumba chake ulifunguliwa na watu wawili waliovalia sare za polisi. Walikuwa wamebebelea bunduki ndogo mikononi mwao.



      “Afisa Kone, upo chini ya ulinzi. Nyanyuka upesi twende kituoni!”



      Kone alijikuta anatabasamu kwa kuchanganyikiwa. Kichwa chake kilifeli kughani mawazo kwa muda. Polisi walimsogelea na kumtia pingu, kisha wakamtwaa na kumpeleka kwenye gari ‘defender’ walilokuja nalo.



      Hawakumweleza Kone juu ya kosa lake mpaka kituoni. Walimsweka rumande na kumwacha mwanaume huyo asijue la kufanya.







      ***









      Yalikuwa yamebakia masaa manne tu kabla ya jeshi la Liberia kuvamia kijiji kinachokaliwa na wanamgambo wa AMAA. Bwana Samweli alikuwa nyumbani kwake kwa muda huo lakini akiwa karibu sana na mawasiliano na kamanda mkuu wa jeshi aliyekuwa anawasiliana vema na vikosi viwili vilivyokuwa vimetumwa kufanya oparesheni ‘tokomeza’.



      Ilikuwa ni majira ya asubuhi inayojongea kabisa kuifuata mchana. Vikosi viwili vya jeshi vilikuwa vipo njiani sasa vikikaribia kuingia ndani ya kijiji hasimu kwa kutumia usafiri wa magari.



      Baada ya lisaa limoja, yakiwa sasa yamekaribia zaidi, magari hayo yalijigawa yakiwa ndani ya mawasiliano. Moja lilielekea upande wa mashariki na lingine likaelekea upande wa magharibi.



      “Kuweni waangalifu sana,” alisisitizia Samweli. Akiwa ndani ya suti nyeusi alikuwa ndani ya sebule yake kubwa akiwa amekunja nne safi. Simu yake ya mezani ilikuwa sikioni mdomoni akitafuna ‘bubblegum’.



      Nyumba yake kubwa ilikuwa imejitenga mbali kabisa na majengo mengine. Eneo lake lilikuwa tulivu lisilo na bughudha wala purukushani za watu. Majengo machache yaliyokuwa kwa mbali nayo pia yalikuwa ni makubwa watu wakijifungia ndani ya uzio na mageti makubwa.



      Baada ya muda mchache, kama dakika zisizozidi tano tangu Samweli atie neno lake la mwisho simuni, mwanaume mmoja aliyekuwa amejifunika uso kwa kinyago cheusi alitokezea ubavuni mwa ukuta wa nyumba ya waziri huyo.



      Alichomoa visu viwili nyuma ya kiuno chake akavirusha kwa walinzi wawili waliokuwa wamesimama getini, visu hivyo vikawakita shingoni na kuwalaza wafu.



      Haraka mwanaume huyo akajongea getini na kugonga geti mara mbili, akafunguliwa na mlinzi mwingine aliyemdaka shingo na kumvunja. Aliingiza ndani miili miwili ya wale walinzi aliowachoma kisu, akafunga geti na kwenda ndani.



      Yote hayo yalifanyika kwa utulivu mno usijue kama kuna chochote kinajiri.



      Mpaka bwana Samweli anaguswa bega lake la kulia, hakuwa anajua kama alivamiwa. Alitazama akamkuta mwanaume ndani ya kinyago cheusi. Mkononi mwake alikuwa amebebelea bunduki ndogo nyeusi mdomowe akiulekezea kwenye kichwa cha Samweli.



      “Haraka batilisha mpango wako kabla sijakutoa roho!” Sauti nzito ilinguruma ndani ya kinyago.





      ***







      “Haraka batilisha mpango wako kabla sijakutoa roho!” Sauti nzito ilinguruma ndani ya kinyago.



      Macho ya Samweli yalitoka kana kwamba vipande vya matango. Moyo wake ulilipuka na pumzi ilianza kukimbia. Ni kwa namna gani mwanaume huyo alizama ndani pasipo yeye kujua? Hakupata majibu. Ama ni jini! Anataka nini kwangu?



      Hofu ilikamata uso wa Samweli na mwili wake ukaanza kujibu mapigo kwa kutetemeka mithili ya kifaranga aliyenyewa na mvua.



      “Wewe nani?”

      “Huna haja ya kujua. Nimesema batilisha mpango wako haraka!” mvamizi aliongea akinyooshea mdomo wa bunduki kwenye simu ya mezani.



      Haraka Samweli akanyanyua simu na kuiweka sikioni.



      “Ukifanya jambo lolote la kipumbavu nitatoboa kichwa chako!” Alitisha mvamizi. Bwana Samweli aliita namba ya mkuu wa jeshi, ilipopokelewa akatoa amri ya kusitisha oparesheni ya uvamizi wa kijiji makazi cha AMAA haraka iwezekanavyo.



      “Mkuu, unasitishaje mpango huu ghafla hivyo?” Aliuliza mkuu wa jeshi.

      “Nimesema rudisha hivyo vikosi haraka!” Samweli akafoka kabla ya kurejesha simu mezani akiilaza kando ya kitako chake hivyo kupelekea simu hiyo kuendelea kuwa hewani.



      “Tayari,” alisema Samweli akimtazama mvamizi kwa macho ya huruma. Mvamizi yule alikuwa mwerevu, alitambua janja ya Samweli. Pasipo kusema jambo, alinyooshea bunduki yake kwenye simu akampa Samweli ishara ya kuikobeka simu ile kwenye kitako chake.



      Samweli alitii, akaweka simu kitakoni. Hapo ndiyo mvamizi akaongea:



      “Unajifanya mjanja siyo?”



      Kabla Samweli hajajibu, risasi ilitoka kwenye mdomo wa bunduki ya mvamizi ikazama ndani ya fuvu lake la kichwa. Tundu kubwa lililozuka kichwani hapo likaanza kuvuja damu pomoni, wakati huo mvamizi akitazama.



      “Kapumzike jehanam!” alisema mvamizi.



      Masaa manne baadae, gari nyeusi, Harrier, muundo mpya iliingia ndani ya nyumba ya bwana Samweli. Ndani yake ilikuwa imembebelea mwanamke mnene mweusi na mtoto mdogo wa kike mwenye umri wa miaka kumi kwa makadirio mepesi.



      Mwanamke huyo alikuwa ni mke wa Samweli na mtoto huyo akiwa ndiye mtoto pekee wa mheshimiwa huyo.



      Walistaajabu kukuta hamna mlinzi hata mmoja getini hali iliyowalazimu wafungue geti wenyewe. Waliingia ndani na hawakuwakuta walinzi vilevile. Mke alipata mashaka, akakamata mkono wa mwanaye.



      Kitu cha kwanza walichokiona baada ya kuingia ndani ya sebule, kilikuwa ni kichwa cha bwana Samweli juu ya meza. Kichwa hiko kilikuwa kimetapakaa damu na kimepatapakaza damu mezani. Kiwiliwili chake kilikuwa kimelala kwenye kochi, nacho kikiwa kimechafuza damu.



      Sebule ilikuwa inanuka damu!



      Mke wa Samweli alipiga kelele kali wakati mwanaye akiachama mdomo kwa bumbuwazi. Alidondoka chini akizirai, mtoto pekee akibakia hajui cha kufanya bali tu kulia na kuchanganyikiwa.









      ***









      Hilo la Samweli kuuawa na kisha kuchinjwa halikuwa siri. Baada ya takribani nusu saa habari iliwasili kwenye masikio ya kiiongozi mkuu bwana Al Saed.



      Wakati huo alikuwa yu ikulu akiwa anangojea kwa hamu mrejesho wa oparesheni ya kutokomeza kijiji kinachowatunza wanamgambo wa AMAA. Ndani ya mkono wake wa kushoto alikuwa amebebelea sigara aliyokuwa anaivuta kwa zamu.



      Bwana Al Saed si mvutaji wa sigara mara kwa mara isipokuwa tu pale anapokuwa ametingwa na mawazo. Tabia hii inajulikana kwa watu wake wote wa karibu. Pindi anapovuta sigara basi anakuwa katika hali tulivu na ahitaji usumbufu wowote.



      Hii aliyokuwa anaivuta sasa ilikuwa ni sigara yake ya tatu tangu aanze kusubiria taarifa za oparesheni ya uvamizi wa kijiji. Alishapigiwa simu mara moja tu na bwana Samweli, na sasa ulikuwa umepita muda mrefu kabla ya kuhabarishwa nini kilichokuwa kinaendelea, ila aliamua kuvuta subira.



      Simu yake ilipoita, aliwahi kuitazama, alidhani ni bwana Samweli. Alikuta ni kamishna wake wa jeshi, akapokea, akapewa taarifa ya kifo cha bwana Samweli.



      Mwili wa Al Saed ulipigwa ganzi kwa muda. Sigara yake ilidondoka chini akiendelea kusikiliza. Simu ilipokata, akanyanyuka upesi na kwenda ndani ya ikulu moja kwa moja mpaka kwenye chumba chake cha mawasiliano. Alifungua tarakilishi yake mpakato akatazama barua pepe. Huko akakuta ujumbe.



      Ujumbe huo ulitumwa mapema sana. Laiti kama angelitazama mapema basi asingelikuwa na haja ya kupewa taarifa ya mauaji ya Samweli na kamishna wake wa jeshi.



      Picha kubwa ya kichwa cha Samweli kikiwa kimekatwa ilijaa kwenye uso wa tarakilishi. Picha hiyo ilikuwa inatisha lakini Al Saed aliitazama. Alipomaliza akasoma na ujumbe uliombatana na picha hiyo:



      “Nilikwambia usithubutu kufanya jambo lolote la kijinga, ulidhani natania.” Ujumbe huo ulitoka kwa Mr. X.



      “Hiyo ni rasharasha tu, Al Saed. Kadiri utakavyoendelea kufanya ujinga ndivyo utakavyoadhibiwa. Tii amri sasa!”



      Al Saed alifunga tarakilishi yake kwa nguvu. Alirejea kule alipokuwa awali akawasha sigara nyingine na kuendelea kuvuta. Alivuta sigara hii kwa hisia sana. Kichwa chake kilikuwa mbali mno kwa mawazo. Aliwaza mambo mengi ambayo aliyakosea majibu. Ila mwishowe kuna mambo akakubaliana nayo na baraza lake la kichwa.



      Kuna watu ndani ya serikali yake, wanaungana na kundi hili la AMAA kwani hao ndio watakuwa wamevujisha mpango huo wa siri. Alijitahidi kuchambua jambo hilo, labda linaweza likawa limeonekana huko nje, akili yake ikagoma kabisa. Aliamini kazi hiyo imesukwa na msaliti.



      Hakutaka kupaparakia hiyo oparasheni, akampigia mkuu wa jeshi na kumtaka mpango huo usitishwe mpaka pale atakapotoa taarifa zaidi.



      “Sawa, mkuu,” aliitikia mkuu wa jeshi. “Tayari wapo njiani kurudi.”



      Magari mawili yaliyowabebelea wanajeshi yalikuwa yanarudi kwa mwendo mkali baada ya mpango wa uvamizi kusitishwa. Yalikuwa ndani ya eneo kame lenye udongo mwekundu na vichakachaka vya hapa na pale. Eneo hilo lilikuwa tajiri kwa vumbi jekundu.



      Baada ya matembezi ya kilomita kadhaa ndani ya eneo hilo jekundu, madereva waliona magari matano mbele yao umbali wa kilomita kama sita. Magari hayo yalikuwa ni makuukuu ila imara yakiwa yamewabebelea watu lukuki kwa nyuma.



      Baada ya kusogeleana zaidi, ndipo wanajeshi wale ndani ya magari yao mawili wakapata kutambua magari yale yalikuwa yamewabebelea wanaume wenye silaha, na tena walikuwa njiani kuwashambulia! Midomo ya bunduki zao ilikuwa imeelekezwa kwao.



      Kabla wanajeshi hawajaanza kujihami kwa kushambulia, walijikuta katika matata mazito baada ya kuanza kupokea mashambulizi mazito tokea nyuma! Hawakufahamu ya kwamba nyuma yao kulikuwa kuna magari matatu yalikuwa yanawafuata. Maadui hao waliweza kutumia vizuri vumbi lililokuwa linatimuliwa na magari ya wanajeshi hao kwa kujificha dhidi ya vioo vya pembeni. Walijipanga katika mstari mmoja wakicheza na vumbi zito. Haikujulikana walijikobeka humo muda gani.



      Risasi zilirushwa kwa fujo kufuata magari ymawili ya jeshi. Risasi hizo zilitokea mbele na nyuma. Wanajeshi hawakuweza kumudu mashambulizi hayo, madereva walishindwa kumudu vyombo, vikakengeuka!



      Kwa uhakiki zaidi, wanaume wale waliokuwa ndani ya magari yale nane kwa idadi, waliendelea kushambulia magari ya wanajeshi wa Liberia mpaka pale yaliposhika moto na kulipuka, ndipo wakatokomea eneo hilo.









      ***











      Ni jioni tulivu ndani ya kipande kidogo cha ardhi ya Guinea.



      Ndani ya jengo kubwa jeupe lililozingwa na wanajeshi watatu getini, sebuleni, alikuwa ameketi bi Fatma; mke wa Kone. Mkononi alikuwa amebebelea glasi maridadi yenye mvinyo mwepesi rangi ya kahawia. Hali yake ya mwili ilikuwa imetengemaa sasa, majeraha usoni yalikuwa kwa mbali, labda kwasababu ya vipodozi.



      Nywele zake zilikuwa zimesukwa na kufumwa vema. Mwili wake ulikuwa umefunikwa na gauni ghali la heshima. Alikuwa ananukia kama bustani. Kila kitu kilikuwa mahala pake; hakika mwanamke alipendeza. Usingeweza kudhani kama ana watoto kadhaa.



      Macho yake yalikuwa yanatazama filamu ya kilatini akiwa amezama haswa. Filamu hiyo alikuwa anaishushia na kinywaji chake maridadi kabisa mkononi. Kwa muda kidogo alikuwa kwenye ulimwengu wa peke yake.



      Wakati filamu hiyo ikiendelea kunguruma, mlango wa sebule ulifunguliwa akaingia mwanaume aliyevalia kanzu ndefu nyeupe na kofia nyekundu. Mwanaume huyo alikuwa mweusi na aliyejaza nyama, uso wake haukuonekana mpaka pale alipogeuza uso kuuacha mlango na kumtazama bi Fatma kwa tabasamu.



      Alikuwa Raisi!



      Bi Fatma alinyanyuka akamkimbilia na kumkumbatia kwa furaha. Walipeana mabusu kabla hawajaachana na kuketi. Walijuliana hali kisha wakawa wanateta hoja za ziada. Wakati huo filamu iliisha na sasa macho na akili ya bi Fatma ikawa kwa Raisi.



      “Nina habari njema kwako,” alisema Raisi.



      Kiu kikaonekana kwenye macho ya bi Fatma.



      “Habari gani hiyo?” aliuliza bi Fatma akijilaza kwenye mapaja ya Raisi. Raisi alichezea nywele za bi Fatma akiongea:

      “Kwanzia sasa hutohitaji tena kuwa na wasiwasi wala mashaka,” alidokeza Raisi. “Hivi tunavyoongea hapa, Kone yupo ndani, na hatotoka kamwe!”

      Bi Fatma akakurupuka toka kwenye mapaja ya Raisi. Alitazama kwa bumbuwazi uso akiwa ameukunja.

      “Unasemaje?”

      “Kone yupo ndani mpenzi,” Raisi alisema kwa tabasamu. “Hatimaye sasa amenipa sababu nzuri sana ya kumweka ndani; kutotii maagizo ya mkuu wa nchi.”



      Akaangua kicheko.



      “Sasa tunaweza tukajivinjari tutakavyo … vipi hujafurahi?”



      Macho ya bi Fatma yalikuwa mekundu. Alimtazama Raisi kwa uso wa kughafirika akisaga meno.



      “Tafadhali, naomba ukamtoe,” alisema kwa sauti ya kutetemeka.



      “Wewe mzima kweli?” Raisi aliuliza. “Nikamtoe nimpeleke wapi? Ina mana bado unataka kuwa naye pamoja na kukutenda yote hayo?”http://pseudepigraphas.blogspot.com/

      “Tafadhali tafadhali, naomba ukamtoe. Akiwepo ndani watoto watapata shida mno. Nakuomba sana.”

      “Siwezi kumtoa,” alisema Raisi. “Unadhani nikimtoa alafu akagundua itakuaje?”



      Si bure Raisi alitilia shaka. Kone hakuwa mtu wa kumpuuza hata kidogo. Kwanza ni mtu anayejulikana kama mmoja wa maafisa weledi serikalini, watu wengi wanamtambua, huo ni mtandao. Pili, ni mwanaume aliyeumbwa kwa mafunzo ya kutumia viungo vyake kujilinda na hata kuutoa uhai wa mtu.



      Rekodi yake ya jeshi si ya kubeza. Si mzuri sana kwenye habari za upelelezi ila ni mwanaume ambaye ana uwezo mkubwa sana wa kumfanya binadamu mwenzake amuogofye. Jambo hili halikuwa linajulikana sana kwasababu Kone si mtu wa maonyesho wala majigambo.



      Sifa zake hizo ndizo zilimvutia Raisi na kumweka mwanaume huyo karibu akimtuma kwenye kazi zake nyeti. Kone ni mtu wa kutunza siri lakini pia mwenye kuzimudu asiyewahi kukata tamaa. Hakuna kazi aliyowahi kushindwa, labda tu kukawia.



      “Nipo chini ya miguu yako. Kone hajakutenda lolote baya, astahili haya kabisa! Amejitolea sana kukufanyia kazi leo unakuja kumlipa kwa kumfunga?”



      Raisi hakutaka kusikiliza, alinyanyuka akaondoka zake kuelekea chumbani.



      Bi Fatma alilia na kusaga meno. Alijiona msaliti asiye na huruma. Kwa muda aliwafikiria wanae na mumewe aliyeko lupango, kifua kikajaa uchungu na hasira. Alikumbuka namna familia yake ilivyokuwa hapo awali, tabasamu na cheko. Akashindwa kuvumilia.



      Ilimlazimu sasa atoroke ndani ya jengo hilo akaikute familia yake. Ndivyo roho yake ilimwambia.



      Ila anatorokaje?



      Alifikiria namna ya kutoroka katika jengo lenye walinzi getini, mawazo yake hayakujipa kabisa. Alikaa hapo sebuleni akiendelea kuwaza na kuwazua mpaka mishale ya saa saba usiku. Hata lepe la usingizi hakuwa nalo.



      Alinyanyuka akafuata dirisha akatazama nje. Aliona wanajeshi wawili wakiwa wanateta na bunduki zao mabegani. Kwa namna walivyokuwa wamesimama hapo usingeweza kudhani kama Raisi yupo ndani. Bila shaka yale yalikuwa ni makazi ya siri ya Raisi. Hata vyombo vya usafiri vilivyokuwemo ndani havikuonyesha kama ni vya mtu mkubwa kiasi hicho.



      Bi Fatma alienda mlangoni mwa chumba alimoingia Raisi, akaita kwa sauti ya chini. Hakukuwa na majibu. Aliporidhia kwamba Raisi hasikii, alitoka ndani ya nyumba kwa kutembea taratibu. Alifungua mlango akatazama usalama, akaona unaridhisha.



      Alizunguka nyuma ya nyumba kwenda ukutani akidhamiria kuruka. Ila kabla hajafanya hivyo, alihisi kuna mtu anamsogelea. Bila kutazama, haraka akapandisha gauni lake juu na kushusha kufuli yake chini.



      Mapaja yake yote yalikuwa wazi. Gauni lake alilolinyanyua lilikomea chini kidogo mwa makalio.



      Sauti ya mwanaume akisafisha koo ilisikika, bi Fatma akaigiza kujifunika kwa aibu. Alikuwa ni mwanajeshi mlinzi aliyebebelea bunduki akisogea kwa tahadhari, lakini tayari picha ya mapaja ya bi Fatma ikiwa kichwani.



      “Kuna tatizo lolote mama?” aliuliza.

      “Hapana,” akajibu Fatma kwa sauti ya puani. “Kwani kuna tatizo afande?” akauliza kichokozi.



      Akili yake yote ilikuwa inaifikiria bunduki ya mwanajeshi ni kwa namna gani ataitia mkononi.







      ****





      Kuna nini kwenye mahusiano ya Raisi na bi Fatma?





      Nini hatma ya Kone lupango?







      “Hapana,” akajibu Fatma kwa sauti ya puani. “Kwani kuna tatizo afande?” aliuliza kichokozi. Alilegeza macho na lips zake alizibinua katika namna ya pekee. Kwa muda mchache sana alifanikiwa kuufanya uso wake kuwa mithili ya mtoto – asiye na makosa na anayevutia, kwa pamoja.



      “Hamna tatizo mama. Nipo tu lindo,” alisema Mwanajeshi kwa sura nyepesi. Bi Fatma alinyanyua miguu yake akamfuata mwanaume huyo akimtazama machoni. Uso wake ulitosha kabisa kumpumbaza mwanaume wa watu aliyekuwa hajui cha kufanya kwa muda huo zaidi tu ya kumtazama.



      “Kuna kitu nataka kukwambia,” alinong’oneza Fatma. Alikuwa sasa anatia huruma na macho yake yalidai kusikizwa. “Ila sidhani kama una kifua.”

      “Niinacho,” alidakia mwanajeshi. “Unaweza tu ukanambia.”

      “Kweli?”

      “Ndio, mama.”



      Fatma alisogea zaidi. Alishika vifungo vya shati la mwanajeshi akimtazama kwa macho ya ashki. Huwezi amini mwanajeshi yule alikuwa tayari ameshaikomaza dhakari yake. Akili yake ilishakimbilia kwenye mapenzi wakati ya Fatma ikiwaza namna ya kutoka eneo hilo haraka kabla kitumbua hakijaingia mchanga.



      Siku zote silaha ya kwanza ya mwanamke kwenye uwanja wa mapambano, ni nguvu ya ushawishi wake kimapenzi. Mungu hakuwapatia nguvu ya misuli, ila pia hakuwanyima namna nyingine ya kusogeza milima, tena katika njia nyepesi kama vile kumuua mbu.



      Damu ya mwanaume ilikuwa inazunguka upesi. Fatma alijikusanya akafyatua goti lake kukita kende za mwanajeshi aliyekunja sura na kulalama kwa maumivu makali kisha akaikwapua bunduki ya mwanajeshi huyo na kumzaba nayo kichwani, akazirai.



      Fatma alitazama kushoto na kulia, hakukuwa na mtu. Mkononi akiwa na bunduki, alikimbia kuufuata ukuta. Aliukwea upesi na kujitupia nje. Alidondoka mithili ya kiroba lakini hakubakia kuugulia maumivu, alinyanyuka na kuondoka kwa kukimbia.



      Akiwa ameacha jengo hilo kwa umbali wa robo kilomita, alisikia filimbi kali iliyomshtua. Aligeuza uso wake kutazama, punde akaona wanaume wawili wanatoka ndani ya uzio. Walikuwa wamebebelea bunduki mikononi mwao wakiteta kupeana maelekezo. Ilikuwa ni wazi wanamtafuta yeye.



      Haraka Fatma alikimbia akielekea upande wa kaskazini. Kwenye kona ya kwanza, aliitupa bunduki, kona yake ya pili akakutana na pikipiki aliyoisimamisha na kukwea.



      “Twende upesi!” aliamrisha.

      “Hii siyo pikipiki ya biashara dada.”

      “We twende! Twende!” Fatma alisema akimpiga dereva makofi ya mgongo.

      “Unaelekea wapi sasa?”

      “We twende tu bwana! – ila siyo huku!” alinyooshea kidole alipotokea.



      Dereva akaondoa chombo chake kwa kasi. Baada ya kuendesha kwa muda kidogo, Fatma akampa maelekezo wapi anataka kwenda. Alielekezea nyumbani kwake.



      “Kuna mtu anakukimbiza dada?” Dereva aliuliza. Fatma alikuwa yu bize kutazama nyuma kama anafuatwa. Uso wake ulikuwa umetwaliwa na hofu. Moyo wake ulikuwa unapiga kwa kasi. Dereva alirudia swali lake mara mbili ndipo akamsikia.



      “Ni wezi tu walikuwa wanataka kuniibia.”

      “Pole sana.”



      Fatma alifika nyumbani akaonana na mlinzi. Alimuuliza kituo alipopelekwa mume wake, akamwambia. Alimkabidhi dereva fedha, akazikataa akidai ni msaada tu. Fatma alikwea tena pikipiki hiyo mpaka kituoni kukutana na mumewe. Baada ya kujitambulisha, aliruhusiwa kuonana na mlengwa wake, ila kwa kishingo upande sana, na tena akipewa muda mchache mno. Laiti kama Kone angelikuwa ni mwananchi wa kawaida, Fatma asingelipata fursa hiyo.



      Alienenda mpaka kwenye chuma za lupango aliyoelekezwa, akazishika na kuita jina la mumewe mara moja kwa sauti ya chini. Kulikuwa ni giza na hakuwa anaonekana yeyote ndani. Mbu walikuwa wamejaa wakisikika wanaimba kwaya.



      Baada ya muda mfupi, vishindo vya miguu vilivuma, na mara Kone akatokeza. Macho yake yalikuwa mekundu, uso wake ulikuwa mzito. Hakudumu ndani ya lupango hata kwa siku mbili ila alikuwa tayari amejaa vipele. Hakula muda wote aliokuwemo humo ndani, hakutaka kabisa. Kichwa chake hakikupata mapumziko dhidi ya mawazo.



      “Nisamehe mume wangu,” yalikuwa maneno ya kwanza Fatma kuyasema baada tu ya kumuona Kone.



      “Najua nimekukosea sana. Hata haya unayoyapitia ni mimi nimesababisha, ila natamani nipate muda wa kurekebisha makosa yangu. Naomba unipe muda wa kunisikiliza, nina mengi ya kusema.”



      Kone hakusema jambo. Kwa kutazama tu uso wake ingetosha kukupa jibu ni namna gani alivyokuwa ameghafirika, amekwazika. Macho yake hayakuweza kuvumilia zaidi, yakaanza kudondosha machozi. Meno yake yaliumana nusura yavunjike.



      “Nisamehe mume wangu. Haikuwa lengo langu, wala haikuwahi kuwa dhamira yangu,” aliendelea kudai Fatma.



      “Watoto wapo wapi?” Kone akauliza.

      “Kwa bibi yao.”

      “Mara yako ya mwisho kuwaona ni lini?”

      Fatma alijiuma kujibu.

      “Nenda kawatazame na ukae na watoto. Sitaki kukuona hapa kamwe!”

      “Siwezi kwenda kuwaona. Na sijui kama nitapata hiyo nafasi, Kone. Inawezekana hata hii ikawa ndiyo nafasi yangu ya pekee kukuona.”



      Fatma alitazama pande zote, kisha akasema kwa sauti ya chini zaidi.



      “Raisi ananiwinda kwa sasa. Hapa nimetoroka toka kwenye makazi yake. Najua ataniadhibu punde tu atakaponikamata. Kwa muda wote huo nilikuwa kwake, nikiishi kama mtumwa …”



      Hakuendelea zaidi, kiganja kikubwa kikamgusa begani.



      “Muda wako umeisha.” Sauti kavu nzito ilinguruma. Alikuwa ni polisi, mwanaume mrefu mweusi. Macho yake yalikuwa yanang’aa kama ya paka. Alimtazama Kone kwa jicho kali kabla hajamsukuma Fatma kuelekea upande wa kutoka.



      Kone hakusema jambo, alibakia pale vyumani akitazama mkewe akiyoyoma. Muda mfupi mbele, masikio yake yakamtaarifu kuna ujio mpya pale kituoni. Walikuwa ni wanaume wawili ambao walijitambulisha kwa sauti za kujiamini, Kone hakusikia vema, ila mwishowe sauti ya polisi, yule aliyekuja kumtwaa Fatma, ilifika vizuri masikioni mwake ikisema:



      “Mnaweza mkamchukua!”



      Fatma alipaza sauti ya kukataa, ila mara sauti ya kofi ikavuma kisha kimya. Mara sauti ya gari nayo inasikika na kisha kutulia. Ni dhahiri shayiri, Kone akawa amejua nini kilichotukia. Aliminya vyuma vya lupango kwanguvu mno. Alisaga meno yake akiwa bado hana cha kusema. Alisimama hapo kwa muda wa kama nusu saa, kichwa chake ndicho kikihangaika huku na kule.



      Mwishowe alihitimisha kwa kusema:

      “Hii ni vita: Aliyelikoroga atalinywa.”

      Aliacha vyuma vya lupango akarudi kule alipokuwa. Gizani.







      ***







      Wakati wa mchana mchanga; Sierra Leone.



      Rose yupo ndani ya nyumba yake kubwa akiwa karibu na dirisha kubwa la kioo. Macho yake yalikuwa yanatazama nje, barabarani, ambapo hakukuwa shwari. Kuna muda watu walikuwa wanaonekana wakipita kimakundimakundi mikononi mwao wakibebelea silaha za jadi.



      Mitaa haikuwa salama kabisa kwa watu kufanya shughuli zao. Tokea maandamano ya wafanyakazi yalipotukia, idadi ya watu waliouawa na kujeruhiwa ilikuwa inaongezeka maradufu. Si wananchi wala wanajeshi na polisi waliokoma kupambana. Huku na kule vurugu zilikuwa zinaripotiwa.



      Tangu asubuhi alipoamka, Rose alikuwa ameketi karibu na dirisha akitazama. Alijaribu kumpigia simu Kone apate kumweleza, ila alikuwa hapatikani. Aliwaza nini itakuwa shida. Kwa namna moja akili yake ikamtaarifu Kone yupo matatizoni. Lakini atamsaidiaje ilhali kutoka tu ndani ya nyumba si salama?



      “Dada!” Sauti ya mfanyakazi wa ndani ilimshtua Rose.

      “Unahitaji chochote?”

      “Hapana, ahsante.”

      Rose aligeuza shingo yake akaendelea kutazama nje, ila mfanyakazi wake hakuondoka.

      “Simu inaendelea kuita, dada,” alisema mfanyakazi kwa sauti ya unyenyekevu. Uso wake ulikuwa mpole akionekana si mjuvi sana wa jiji, ila ndani ya sare alipendeza.

      “Nani anapiga?”

      “Yule yule!”

      Rose alisonya kisha akanyoosha mkono wake, mfanyakazi akampatia simu. Alikuwa ni Talib anapiga. Aliitazama simu akifikiria, mwishowe akapokea.



      “We mwanamke kwanini napiga simu muda wote hupokei!” Sauti ya Talib ilifoka saizi ya kuumiza masikio.



      “Simu ilikuwa mbali,” Rose akajibu kiwepesi.

      “Simu ilikuwa mbali tokea juzi?” Talib aliuliza. Rose akakata simu na kuizima kisha akaendelea kuangaza macho yake nje ya nyumba, huko barabarani.



      Haikupita muda mrefu msafara mzito wa Talib ukafika mbele ya nyumba ya Rose. Wanajeshi kibao wakiwa wamebebelea bunduki walitapakaa huko nje kuhakikisha usalama.



      Talib, kwa kasi kubwa, aliingia ndani ya nyumba ya Rose akipaza sauti kumuita mwanamke huyo. Uso wake ulibebelea hasira nzito, hata hatua zake zilisema hivyo. Alimtafuta Rose sebuleni pasipo mafanikio. Akaenda chumbani. Huko akamkuta Rose ameketi kitandani.



      Kwa namna Talib alivyokuwa amevaa, nguo za jeshi, msako wake ulikuwa ni kama vile anamsaka hayawani, ama msaliti wa taifa.



      “Hivi we mwanamke, nini kinakupa jeuri kiasi hiki?” Talib alifoka.



      Rose alimtazama mwanaume huyo kwa uso wa utulivu. Akili yake ilimtahadharisha mapema kwamba ujio ule haukuwa wa amani, hivyo upesi akaanza kufanya jitihada za kujihami. Jitihada hizi Talib hakuwa na taarifa nazo.



      “Si nakuuliza wewe!” Talib aliendelea kufoka. Aliufunga mlango kwa kuubamiza kisha akaanza kumfuata Rose akikunja vema mikono ya shati lake.

      http://pseudepigraphas.blogspot.com/

      “Naona huna adabu, unataka kunipanda kichwani. Sasa leo nitakuonyesha upande wangu wa pili.”



      Kabla hajamgusa mwanamke huyo, alijikuta yupo chini baada ya kubamizwa kichwani kwanguvu na taa ya mezani. Alidondoka chini kama kiroba. Macho yake yalikosa nguvu, akawa haoni kabisa. Kichwa kiligonga kwa maumivu makali mno. Upande wa kushoto wa uso wake alipasuka, damu ikawa inavuja.



      Ilimchukua kama dakika kumi kurejea katika hali ya ahueni. Alinyanyuka akiwa ameshikilia kichwa chake, na uso ameukunja. Alitazama huku na kule, hakumuona Rose! Alitazama dirisha akaliona li wazi. Haraka alitoka chumbani akawapasha habari walinzi wake wamtafute Rose popote pale alipo. Aidha akiwa hai au amekufa, anataka amwone.



      Upesi wanajeshi kadhaa walisambaa mtaani kumtafuta Rose. Talib alirejea ndani ya nyumba akaketi sebuleni. Bado alikuwa ameshikilia kichwa chake katika namna ya kuugulia maumivu.





      ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog