Search This Blog

Sunday 20 November 2022

VIPEPEO WEUSI: FROM ZURICH WITH RULES - 1

 





    IMEANDIKWA NA : THE BOLD



    *********************************************************************************



    Simulizi : Vipepeo Weusi: From Zurich With Rules

    Sehemu Ya Kwanza (1)





    VIPEPEO WEUSI



    SEASON 2 - FROM ZURICH WITH RULES



    EPISODE 01



    BARABARA INAYOELEKEA KWENYE MAKAZI YA WAZIRI MKUU – MLIMWA, DODOMA



    “Ili kuweka kumbukumbu kwa usahihi zaidi naomba urudie tena kujitambulisha..!” yule binti mrefu mwenye suti nyeusi akaongea tena kwa mara nyinine.



    “..hivi tutarudia hii kwa mara ngapi ili uridhike.!” Nikajitahidi kumuuliza kwa kujifanya kukereka haswa, lakini ukweli ni kwamba akili yangu na macho yangu vyote vilikua kwenye mlango wa gari ulio wazi kama mita tano kutoka pale tulikosimama.



    Giza nene na mwanga wa taa ya kurekodia video uliokuwa unanimulika usoni ulinifanya nisiweze kuona sawia kile ambacho nilitaka kukiona ndani ya gari. Japokuwa sikuweza kuona kwa usahihi niliotamani lakini katika pua zangu niliweza kabisa kusikia harufu ya damu mbichi ya binadamu, na haikuwa damu mbichi tu bali ilionyesha kabisa ilikuwa ni damu mbichi inayoendelea kutiririka kutoka kwenye mwili wa binadamu aliye hai.



    “…tutarudia mara nyingi kadiri ambavyo utaendelea kunizungusha.!” Yule dada naye akaongea kwa ukali kiasi na safari hii kunifanya nihisi hisia ya kukereka kwenye sauti yake.



    Sikumjibu chochote moja kwa moja, akili yangu na macho yangu bado vilikuwa kwenye ule mlango wa gari mbele yetu. Nikaanza kuhisi labda huyu binti hajui mwenzake yuko katika hali tete kiasi gani. Lakini kwa kadiri nilivyomsoma juu ya weledi wake wa matumizi ya silaha ilinifanya niondoe hisia za kudhania kuwa labda binti huyu alikuwa hajui hali tete aliyonayo mwenzake pale kwenye gari. Silaha ambayo nilitumia kufyatua risasi aliiona na ilikuwa pale ndani ya gari, bastola aina ya glock 19 na nilikuwa na uhakika kabisa alikuwa anajua madhara ambayo bastola hii inafanya kwenye mwili wa binadamu ikifyatuliwa umbali wa karibu kaka ambavyo mimi niliifyatua.



    “…mwenzako kama hatutampatia huduma ya kwanza ndani ya dakika chache zijazo tutampoteza.!” Nikaongea tena kwa mara nyingine huku bado macho yangu nimekaza kuelekea kule ambapo mlango wa gari ulikuwa umefunguliwa.



    Nadhani safari hii alikuwa amegundua jinsi ambavyo nilikuwa nahangaika na kujitahidi kukaza macho kuelekea lilipo gari. Hakunisemesha chochote kile, akageza ile taa ya kurekodia video na kumulika pale mlangoni kwenye gari. Hisia zangu na harufu ya damu niliyokuwa naisikia puani kwangu sikuwa nimekosea, Yule dada wa kizungu bado alikuwa anaendelea kuvuja damu. Lakini jambo ambalo lilinishangaza ni kwamba, alikuwa amejishika maeneo ya karibu na kifua huku damu zikibubujika na pale pajani ambapo nilimlenga kulikuwa nako kunatoka damu lakini haikuwa damu nyingi kama ile niliyoiona inatoka pale juu karibu na kifua ambakoa alikuwa amejishika. Nilipofyatua risasi nilikuwa nimemlenga pajani kwa makusudi kabisa nikiwa na lengo la kumsababishia jeraha kubw lakini asipoteze uhai. Kabla ya huyu mwenzake kugeuza taa na kunimulikia pale kwenye gari niweze kuona, nilipo kuwa awali bado nahisi tu kwa kusikiliza harufu ya damu puani kwangu na nilipong’amua kwamba damu ilikuwa bado inaendelea kutiririka kwa binti huyu wa kizungu, kichwani mwangu nilikuwa nimehisi labda nilipomlenga pale pajani nilikosea na kupasua mshipa mkuu wa ateri na ndio maana nilisikia harufu ya damu mbichi inayobubujika kutoka kweny mwili, lakini kumbe hisia zangu hazikuwa sahihi, binti wa kizungu alikuwa pia anabubujikwa na damu kutoka kwenye kifua.







    Lakini nilikuwa nakumbuka kwa usahihi kabisa kuwa nilifyatua risasi moja tu na nililenga pajani. Kama kumbu kumbu yangu ikomsahihi, kwa nini huyu binti wa kizungu ameshikilia mikono kifuani huku anavuja damu?



    Nikainua kichwa kumuangalia tena Yule mwenzake, binti mrefu, mweusi ambaye alikuwa ananirekeodi video muda wote huu na akinikera kwa kutaka niongee kitu kile kile tena na tena akidai kwamba bado sijaeleza kwa ufasaha vile anataka. Ilikuwa ni kana kwamba muda wote huu alikuwa ananisoma kile ambacho nilikuwa nakiwaza kichwani mwangu, kwa sababu nilipogeuza shingo tu na kumuangalia nilimkuta ameganda ananikodolea macho akionyesha dalili kuwa aklikuwa ananiangalia hivyo kwa muda mrefu sana. Akageuza tena ile taa ya kurekodi video na kuwasha tena camera ya vieo ili tuendelee kurekodi .



    “…je ne…peux…pas…respirer..!” (siwezi kupumua)



    Sauti ya Yule binti wa kizungu ililalamika kwa taabu sana kutoka pale kwenye mlango wa gari uliofunguliwa.



    “…etre fort Ilana..” (vumilia Ilana)



    Huyu binti mwingine akamjibu mwenzake kwa kifarasa chenye lafudhi ya Rwanda bila kugeuka kumtazama mwenzake, bado alikuwa ananiangalia mimi kwa kunikazia macho.



    Kwa hakika kabisa nikaelewa huyu binti ni mtu wa weledi na likuwa anajua anachokifanya na alikuwa tayari kuhatarisha kila kitu kama sitataka kukubaliana na kile anachonieleza. Nikapiga hesabu ya haraka haraka kichwani. Hapa tulipokuwa tumesimama ni umbali wa kama mita mia moja tu kutoka katika barabara binafsi inayoelekea kwenye makazi ya Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungani wa Tanzania na tulikuwa tumebakiza kama kilo mita mbili tu kutoka hapa tulipo mpaka kufika kwenye makazi ya Waziri Mkuu. Kama tutaendelea kuzozana hapa nilikuwa naona hatari mbili mbele yetu. Hatari ya kwanza ni huu mwanga wa taa ya kurekodia video aliouwasha huyu binti unaweza kugundulika na Wanausalama wanaomlinda Waziri Mkuu kule walipo jee sehemu ya mwinuko wanayoiita Mlimwa. Lakini pia hatari ya pili niliyokuwa naiogopa zaidi ni Yule binti wa kizungu anayevuja damu, akiendelea kuvuja damu vile kwa dakika kadhaa zijazo basi hakuna shaka kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kumpoteza.



    “Ok! Unatakaje?” nikamuuliza yule binti.



    “nataka utambulisho ulio sahihi zaidi ndio uingie kwenye kumbukumbu.!” Akanijibu kwa hasira kwa Kiswahili kilichojaa lafudhi ya kinyrwanda.



    “sawa!” nikmuitikia tu kwa kifupi.



    Sijui ni muda gani alizima tena kamera, lakini nikamuona kwa mara nyingine tena anaiwasha kamera na kasha kuniangalia kuashiria kuwa yuko tayari niendelee na ninachopaswa kukifanya.



    “Jina langu naitwa Rweyemamu Charles Kajuna, watu wa karibu wanapendelea kuniita Ray na marafiki zangu wanapendelea kuniita jina la utani ‘Kichwa’… hii ni recording namba 004W22 kuthibitisha kuwa ninayo mkononi mwangu password ya sanduku 7712/LH lililopo Union Bank Of India, jijini Mumbay nchini India. Narudia hii isomeke kama recording namba 004W22.!”



    Nikamaliza na kumuangalia usoni yule binti huku nimeamkazia macho, “Umeridhika?” nikamuuliza nikiwa nimekereka haswa.



    “Angalau inaridhisha kwa utambulisho.!” Akanijibu huku kwa mara ya kwanza nikimuona akitabasamu.



    “…jene.. peux… pas… respirer..!!” (siwezi kupumua)



    Sauti yenye kugugumia kwa maumivu ya yule binti wa kizungu ililalamika tena.



    “..ca va! Je suis ici Ilana.!” (Usijali.! Niko nawe hapa Ilana) Yule binti mweusi mrefu akamjibu mwenzake akikiongea kifaransa kwa lafudhi ya Kinyarwanda.



    Akaanza kukusanya kusanya vifaa vyake vya kurekodia, yaani kamera, taa, stendi ya kamera na vitu vingine na kisha nikamuona ameviweka kwenye mfuko wa plastiki, kisha akaweka kwenye mfuko mwingine tena wa pastiki lililoonekana kuwa gumu zaidi na kisha kuviweka vitu vyote kwenye begi la mgongoni ambalo lilikuwa kando yake. Alikuwa anafanya zoezi hili haraka haraka kana kwamba anafanya kitu hiki kila siku. Muda wote huu ambao alikuwa anakusanya vifaa vyake nilikuwa nimesimama tu pale pale ambako nilikuwa nikimuangalia yeye lakini akili yangu yote ilikuwa kwa yule binti wa kizungu anayegugumia kwa maumivu.



    Baada ya kumaliza kuweka kila kitu chake kwenye begi, kwa haraka sana akageuka na moja kwa moja kwenda pale kwenye mlango wa gari uliofunguliwa. Akarusha begi ndani ya gari na kisha kumuinua mwenzake kutoka kwenye gari na kumlaza chini kwenye ardhi. Alikuwa anafanya kila kitu kwa haraka haraka sana kana kwamba mwenzake huyu ndio kwanza amemuona muda huu majerajha yake. Nikavuta picha dakika chache tu zilizopita jinsi ambavyo nilikuwa nikimsisitiza kuhusu mwenzake na alivyokuwa anajikaza kutoonyesha hisia kana kwamba alikuwa hamuoni mwenzake.



    Sasa hivi ndio nilikuwa nimepata wasaa mzuri zaidi wa kuisogelea ile gari yao na kuichunguza kwa makini zaidi. Ilikuwa ni Range Rover nyeusi ambayo kwa kuiangalia kwa haraka haraka nilihisi kwamba ilikuwa ni toleo la zamani kidogo japo sikuweza kujua ni toleo la mwaka gani hasa. Nikatupa jicho kwenye namba za gari na haraka haraka nikazikariri kichwani, “T338 CNL”. Kila ambapo nilijaribu kutupa jicho ndani ya gari ili kujaribu ufahamu labda kama kuna chochote kile cha muhimu ili nikifahamu lakini kutokana na giza kubwa na taa za ndani ya gari kuzimwa sikuweza kuona chochote kile. Lakini japokuwa sikuweza kuona kitu chochote ila kutokana na mlundikano wa ile sehemu ambayo yule binti alirusha begi ndani ya gari, nilikuwa na uhakika kabisa ndani ya gari kulikwa na zaidi ya begi lile moja lililowekwa muda huu.



    “..jene…peux… pas…repsirer..!”



    Nikamsikia tena yule binti wa kizungu analalamika pale chini ambako amelazwa na mwenzake. Bado alikuwa analalamika kwamba hawezi kupumua. Mwenzake nikamuona ameongeza juhudi ya kujitahidi kufuta damu kifuani huku anajitahidi kuzuia damu isiendelee kutoka.



    Ilibidi niiname pale chini alipolazwa yule binti wa kizungu ili niweze kuona kwa usahihi zaidi ni kiasi gani alikuwa ameumia. Kilichokuwa kinanishangaza zaidi ni kwamba nakumbuka nilimpiga risasi pajani kwa makusudi kabisa ili nisimuue, lakini sasa namshuhudia akiwa anavuja damu kifuani.



    “kwa nini anatokwa na damu kifuani?” nilimuuliza yule binti wa kinyarwanda baada ya kuinama pale chini na kujiridhisha kuwa ni sahihi kabisa macho yangu yalikuwa haayanidanganyi. Alikuwa anavuja damu kifuani.



    “Swali gani hilo… Idiot! Si umempiga risasi.!!” Yule binti wa kinyarwanda alifoka huku anaendelea kumfuta damu mwenzake.



    “Yeah.!! Najua nimempiga risasi, lakini haikuwa kifuani… nilimpiga pajanii.!” Na mimi nikafoka.



    “alidondoka kwenye kisiki cha mti kikamchoma kifuani baada ya kumpiga risasi pajani.!” Alinijibu bila kuniangalia akiendelea kufuta damu mwenzake.



    Niakelewa sasa kwa nini yule binti wa kizungu alikuwa analalamika kuwa alikuwa anshindwa kupumua. Ila kilichonishangaza zaidi ni kwanini huyu binti wa kinyarwanda alikuwa hajaelewa kile ambacho mimi nimekigundua. Huyu binti alikuwa anaonekana dhahiri kabisa kwamba alikuwa na uzoefu wa mikiki mikiki ya matukio ya namna hii, lakini ajabu ni kwamba alikuwa haoni kile ambacho nilikuwa nakiona. Kichwani nikanza kupata shaka kidogo kama huyu binti ndiye yeye haswa ninaye mfikiria ndiye na anavyojitahidi kunionyesha kuwa ndiye.



    “Nadhani hicho kisiki cha mti kilichomchoma kilifika mpaka kwenye pafu na naamini kuna damu imeingia pafuni ndio maana anashindwa kuhema.!’ Nikamueleza huku namsukuma taratibu kwa mkono ili asogee pembeni nijaribu kusaidia kuokoa uhai wa yule binti wa kizungu.



    “Una kisanduku cha huduma ya kwanza?” Nikamuuliza huku napapasa pale kifuani kwa yule binti wa kizungu ambapo amejeruhiwa.



    Yule binti wa Kinyarwanda akainuka bila kunijibu chochote na kuelekea kwenye gari. Niliendelea kupapasa pale juu ya kifua cha yule binti kwenye kidonda mpaka nikagusa nilipo pataka. Kati kati ya kidonda pale kifuani kilikuwa na kipande cha mti kimekatikia.



    “hii hapa.!” Yule binti wa Kinyarwanda alikuwa amerejea na briefcase ambayo alipoifungua ilikuwa imesheheni vifaa mbali mbali vya kidaktari na madawa.



    Nikapekua pekua na kuchukua bomba la sindano. Nikachana kifungashio chake cha plastiki na kisha nikaondoa ile sindano ya mbele inayotumika kuchoma kwenye nyama. Pia nikaondoa mshikio wake wa nyuma ambao unatumika kuvuta dawa kutoka kwenye chupa ya dawa na kisha kubonyezwa ili kusukuma dawa kwenda kwa mtu anayechomwa. Mshikio huu nao niliuondoa pia. Kwa hiyo lilikuwa limebaki bomba tupu liko wazi pasipo sindano yake ya mbele na pasipo mshikio wake wa nyuma.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Nilichokuwa nataka kufanya ni kuondoa ile damu ambayo nilikuwa naamini kabisa imeingia ndani ya pafu na kulijaza na ndio maana binti huyu wa kizungu alikuwa analalamika kuwa anashindwa kupumua. Mapafu yenyewe yana asili ya kuwa na “presha” innayosukuma kitu kutoka nje yake. Kwa hiyo nilikuwa nataka kutumia nadharia hiyo kuingizia bomba hili tupu la sindano ili kulipa pafu uwezo wa kusukuma damu hiyo iliyoingia kutoka nje na nilikuwa nataka kutumia bomba la sindano kwa kuwa japo nimeondoa sindano pale mbele lakini bado kuna mdomo mwembaba unaoshikilia sindano pale mbele, ambao mdomo huu ndio hasa nilikuwa nataka kuutumia kuuzamisha ndani ya pafu.



    “Mshikilie mikono.!” Nikamueleza yule binti wa kiinyarwanda.



    “Unataka kufanya nini?” Yule binti akaniuliza kwa mshangao mkubwa huku ametumbua macho.



    “Nimekwambia mshike mikono.!” Nikamfokea.



    Safari hii hakunishia tena, akamshika mwenzake mikono na kwa kuigandamiza chini kwenye ardhi kama vile tulikuwa tunataka kumchinja. Na mimi nikakaa upande wa miguu katika namna amabyo nilikuwa nimetumia miguu yangu kugandamiza chini ardhini miguu ya yule binti wa kizungu.



    Japokuwa hapa tulipo kuliwa na giza totoro lakini macho yetu tayari yalikuwa yamezoea hali ile ya giza kwa hiyo kwa kiasi fulani tulikuwa tunaonana kwa ufasaha kabisa. Nilikuwa namuona yule binti wa kizungu jinsi alivyo nikodolea macho kwa uoga bila kujua ni nini nilichokuwa nataka kukifanya.



    “Ilana… this is going to hurt!” nikamueleza kwa kingereza yule binti huku namuangalia machoni.



    Akaniitikia kwa kutikisa kichwa akimaanisha kuwa ananiruhus kufanya kile ambacho nilikuwa nataka kufanya. Moja ya udahifu wa asili wa binadamu, tumaini lolote linaokuwa mbele yetu linakuwa ni tumaini bora kuliko kutokuwa na tumaini kabisa.



    Nikapapasa tena pale kwenye kidonda chake mpaka niliposhika sawia kile kipande cha mti kilichokatikia kifuani na kwa haraka nikakichomoa na kwa kasi ya ajabu nikachomeka lile bomba la sindano pale pale nilipochomoa kipande cha mti.



    “Aaaaaaaaaaaaaaaaaaa..!!!”



    Yule binti wa kizungu alilia kwa nguvu kwa sauti ya maumivu ya hali ya juu. Damu ilikuwa inaruka kutoka kwenye lile bomba la sindano nililochomeka katika nmana ya kufanana kabisa na mtu anapojaza maji mdomoni na kisha kuyapuliza nje kwa nguvu. Hali hii ilidumu kwa muda wa kama sekunde ishirini hivi kisha damu ikaacha kuruka.



    Mwenzake yule binti wa Kinyarwanda alikuwa ametumbua macho kwa woga huku jasho linamtoka. Alionekana dhahri kabisa hakuwa amezoea kuona damu ikimwagika hivi au kumuona mtu kwenye maumivu makali kiasi hiki. Nilijikuta nazidi kupata shaka kama binti huyu ndiye ninayemfikiria kuwa ndiye.



    Yule binti wa kizungu alikuwa anahema juu juu kama alikuwa anakimbia kupandisha mlima kwa masaa kadhaa. Taratibu akaanza kurejea kwenye hali ya kawaida na hata kuhema nako akawa anahema kawaida.



    “..merci beaucoup…merci … merci.!!” (Asante sana…asante… asante.!!)



    Yule binti alikuwa anashukuru huku ana hema akionekana kupata haueni sasa.



    Nikamsafisha kidonda chake na kisha kukifunga vizuri kwa bandeji, na pia nikafanya vivyo pale pajani ambapo nilimpiga risasi. Baada ya hapo mwenzake akambadili nguo na kisha wote tukaelekea kwenye gari.



    Yule binti wa Kinyarwanda likuwa ameketi kwenye usukani, mimi nimeketi kwenye siti ya mbele ya abiria na yule mwenzake ameketi peke yake siti ya nyuma.



    Tulikuwa tumeketi kwenye hali ya ukimya kwa takribani dakika tano nzima kila mmoja akitakari namna ya kuanza kwa maongezi haya baada ya mwanzo mbaya wa awali.



    “Jina langu naitwa Giselle Pie….”



    “Nakufahamu wewe ni nani… Giselle Jean Pierre… uko hapa kwa niaba ya LE BLOC..!!” nilimkatiza yule binti wa Kinyarwanda kabla hajamaiza senetesi yake.



    “lakini huyu mwenzako ndiye mgeni machoni mwangu japo naamini yeye ndiye mwenye namba ya sanduku la Zurich.” Niliongea huku nageuka nyuma kumuangalia yule binti wa kizungu.



    “..je m’appelle Ilana Dario… suis ici au nom du president de Citibank.!” (jina langu naitwa Ilana Dario niko hapa kwa niaba ya rais wa Citibank). Yule binti wa kizungu naye akajitambulisha.



    “I’m sorry I shot you.!” (samahani nimekupiga risasi) nikamuomba msamaha kwa sauti ya kinafiki kabisa.



    “Baise toi.!” Yule binti wa kizungu kwa hasira akanitukana tusi la nguoni, ‘f*ck you.’



    Binti wa Kinyarwanda, Giselle nikamuona anatazama saa kwenye kiganja cha mkono. Japokuwa kulikuwa na giza ndani ya gari lakini kwa namna fulani alionekana kuona alichokuwa anatazama mkononi.



    “tumebakiwa na dakika kumi na tano pekee… una kila kitu tunachohitaji?” Giselle aliniuliza.



    “Kila kitu kiko sawa upande wangu.. sijui nyinyi.?”



    Hakunijibu chochote kile. Akawasha gari na tukaanza kutoka porini kukamata barabara inayoelekea kwenye makazi ya Waziri Mkuu.



    Alipoawasha gari ndipo nilipopata wasaa mzuri zaidi wa kupepesa macho mule ndani ya gari. Kwenye siti ya nyuma pembeni kwa Ilana ambako aliweka lile begi lenye vifaa vya kurekodi video kulikuwa na mabegi mengine mawili ya mkononi yakiwa yamejaa vitu fulani ambavyo sikuweza kuvitambua kwa haraka. Lakini juu ya mabegi haya mawili zilikuwa zimewekwa bastola mbili ambazo kwa kuziangalia kwa haraka niling’amua kuwa zote mbili zilikuwa ni “9mm” huku moja ikiwa ni Berette na nyingine ikiwa aina ya Heckler.



    Nilikuwa nakumbuka dhahiri kabisa tangu mara ya kwanza nawaona mabinti hawa wananifuatilia hawakuwa na silaha mikononi na kwa kuzingatia kuwa walikuwa wamenifuatilia kwa zaidi ya dakika arobaini na atano au zaidi ni lazima walikuwa wanafahamu kuwa nilikuwa na silaha. Swali ambalo lilikuwa linajirudia rudia kichwani mwangu ni kwanini walicha silaha zao na kuamua kukabiliana nami bila silaha ilhali wakijua fika kuwa nilikuwa na silaha.



    Kichwani nilizidi kuwa na sintofahamu nikihisi kwamba kulikuwa na uwezekano mkubwa wa kitu fulani nyuma ya pazia kinaendelea tofauti kabisa na nilivyokuwa nafikiri. Maana mwanzoni tayari Giselle alikuwa amenitia shaka baada ya kushindwa kung’amua kuwa mwenzake alikuwa na damu imejaa kwenye pafu hivyo kumfanya ashindwe kuhema sawa sawa. Lakini pia uoga wake alioonyesha kipindi ambapo nilikuwa namtoa mdamu mwenzake Ilana kwa kutumia bomba la sindano. Na sintofahamu ya tatu ilikuwa ni hizi silaha mbili zilizowekwa siti ya nyuma. Kwa nini waliziacha kabla ya kukabiliana na mimi. Hisia yangu hii ya kwamba kuna jambo la zaidi linaendelea hapa tofauti na ninavyodhani ilizidi kupata nguvu zaidi kichwani mwangu.



    Tulikuwa tumeendesha kama mwendo wa dakika tano nzima kuelekea kwenye makazi ya waziri mkuu ndipo ambapo tulisimamishwa na gari ya kwanza ya maaskari wanaolinda maeneo yanayozunguka makazi ya Waziri Mkuu.



    Ilikuwa ni gari aina ya ‘Difenda’ iliyo wazi nyuma, ambayo ilipakia nyuma maaskari wanne huku mbele kukiwa na askari wawili.



    Mara tu baada ya kutusimamisha walishuka maaskari wawili waliovalia makoti marefu ya doria, na moja kwa moja wakaja mpaka kwenye gari letu. Hawakutuuliza kitu chochote kile wala kutusalimu, walitumulika tu tochi usoni kila mmoja wetu na kisha wakaturuhusu kuendelea na safari yetu kuelekea kwenye makazi ya Waziri Mkuu. Kitendo chao kile cha kutotuhoji chochote na kuturuhusu tuende kiliashiria kwamba walikuwa wamepewa taarifa kuhusu ujio wetu na walikuwa wanatutegemea.



    Tuliendesha gari kwa takribani dakika tano nyingine ndipo tulipoingia hasa kwenye mandhari ya eneo hili la Mlimwa. Eneo hili liko katika mwinuko mkubwa kiasi kwamba ukifika hapa naa kutazama nyuma yako unaweza kuuona mji wote wa Dodoma mjini kwenye upeo wa mcho. Kwa kaisi fulani lilikuwa ni eneo ambalo limejitenga mno na hakukuwa na nyumba yoyote nyingine ndani ya kipenyo cha kilomita tatu.



    Tulikuwa hatimaye tumefika mbele ya geti kuu la kuingia kwenye makazi haya adhimu kabisa. Makazi haya yalikuwa yamezumgukwa na ukuta mkubwa wa urefu wa kama mita tano hivi ukiwa na senyenge za umeme juu yake pamoja na taa kubwa juu ya ukuta kila mahali. Pia upande wan nje wa ukuta nako kulikuwa na maaskari kila baada ya hatua kadhaa ambao walikuwa wanafanya doria.



    Ajabu ni kwamba hata askari hawa wa doria nao hakuna yeyote kati yao ambaye alijishughulisha nasi. Nao dhahri kwamba walikuwa na taarifa juu ya ujio wetu.



    Baada ya kufika tu getini, geti likafunguliwa na gari yetu kuingia. Ndani ya geti upande wa kushoto kuna kijichumba kikubwa cha ulinzi ambacho kwa haraka niliona maafisa usalama watatu ndani yake ambao wote walikuwa wamevalia sare za kijeshi lakini zenyewe vikiwa na rangi fulani kama kijivu.



    “Passcode?” Afisa mmoja ambaye alikuwa nje ya kile kijichumba aliuliza huku anatazama ndani ya gari yetu.



    “December 19”Nikamjibu kwa kifupi.



    Akatuonyesha kwa mkono muelekeo ambao tulikuwa tunapaswa kuufuata kwa ajili ya kupaki gari yetu.



    Ndani ya makazi haya ya Wziri Mkuu, ukiingia tu getini upande wa kulia kuna jengo la ghororofa moja ambalo ni ofisi rasmi ya Waziri Mkuu na Idara zake za usaidizi wa majukumu yake. Alafu katikati kuna eneo kubwa la wazi lenye bustani murua kabisa. Upande wa kulia ndiko ambako kuna makazi ya waziri Mkuu ambayo anaishi yeye na familia yake.



    Sehemu ambayo tulionyeshwa kupaki gari ilikuwa ni mahali fulani nyuma ya kijichumba kile cha ulinzi.



    Mpaka muda huu nilikuwa sikujua ni kwanini lakini hisia zangu zilikuwa zinaniambia kuwa hali ya ulinzi ndani ya makazi haya ilikuwa ni ulinzi mwepesi tofauti na nilivyokuwa natarajia. Nilibaki kujiuliza maswali kichwani kama hali hii iko hivi kila siku au ni leo tu, na jibu lilikuwa linanijia kichwani kwamba ni leo tu hali hii iko hivi. Kila jibu hili liliponijia kichwani kwamba ni leo tu hali hii iko hivi, nilijikuta napata swali lingine la kwanini ulinzi uwekwe mwepesi siku ya leo.



    Tofauti na desturi ya sehemu za makazi za viongozi wakuu wote ambazo nimewahi kufika, hapa kwa Waziri Mkuu hatukusachiwa sisi wala gari yetu kupekuliwa kabla ya kuingia na hata baada ya kuingia. Nilijua pia kuwa huu ni “upendeleo” fulani tu kwa ajili yetu sisi. Kwa mtu mwingine angeweza kuhisi labda hii ni heshima kubwa tulikuwa tunapewa lakini binafsi nilihisi kuna swala ambalo linaendelea nyuma ya pazia.



    Tulishuka kwenye gari na afisa mmoja wa usalama alikuja kutuongoza kuelekea kwenye jengo ambalo Waziri Mkuu anaishi na familia yake. Tulifunguliwa mlango mkubwa wa mbele uliotengenezwa kwa mbao adimu na nakshi za kimanga, mlango ulifungukia ndani ambako moja kwa moja tulikutana na sebule kubwa sana yenye viti vya masofa ya gharama ya hali ya juu. Hakika yalikuwa na mnadhari hasa ya kuishi Waziri Mkuu wa nchi. Hapa sebuleni nako nilishangaa hakukuwa na hata mtu mmoja wa usalama kama ambavyo nafahamu inapaswa kuwa. Kichwani ile hisia yangu kwamba kuna kitu hakiko sawa ilizidi kukua.



    Yule afisa usalama aliyetusindikiza kutuleta hapa sebuleni kutoka kwenye gari alikuwa ameshaondoka na hapa kwa sasa tulikuwa tunakarimiwa na Bibie Sarah Shomari, msaidizi maalumu wa Waziri Mkuu ambaye tulimkuta ameketi kwenye sofa na aliinuka mara tu alipotuona tunaingia. Huu ni mwaka wa pili tangu nimfahamu Sarah lakini leo hii uso wake nilikuwa nauona wenye uchangamfu kuliko siku yoyote ile. Mara zote ambazo nimewahi kukutana naye uso wake huwa unamuonekano wa kikazi. Sio mtu wa utani wa reja reja au maongezi madogo, unapokutana na Sarah Shomari unakuwa umekutana na mtu mwenyekuzingatia weledi wa kazi yake na kila sentensi ambayo itatoka kinywani mwake ni kuhusu kazi na jambo husika lililo mezani. Lakini siku ya leo Sarah alikuwa anatabasamu kana kwamba ni muhudumu wa mapokezi ya hoteli na sisi tulikuwa ni wateja wake.







    “Welcome guys… Sarah Shomari, Personal Assistant to te Prime Minister.!” Sarah alijitambulisha kirafiki kabisa huku anampa mkono Giselle akitumia neno la reja reja “guys” kuonyesha ukarimu wake.



    “Giselle Jean Pierre… LE BLOC.” Giselle alijitambulisha huku naye akimpa mkono Sarah.



    “Ilana Doria… Citibank” Ilana naye akajitambulisha huku anampa mkono kwa taabu Sarah kutokana na maumivu ya kidonda chake pale kifuani.



    “Ilana?? Are you ok?” Sarah akamuuliza kirafiki Ilana baada ya kumuona ananyoosha mkono kwa taabu sana.



    “She had a small ‘accident’ few minutes ago.!” Giselle alidakika kueleza hali ya Ilana huku akitumia vidole kuonyesha hewani alama za kufungua na kufungua usemi, “…….” Alipotaja neon ‘accident’.



    “oooohh so sorry Ilana.!” Sarah akongea akionyesha kuelewa maana ya Giselee kutumia zile alama za funga na fungua usemi hewani.



    Kabla sijajitambulisha, Sarah alinigeuka na kuniangalia huku anatabasamu, “and ofcourse Ray, The Kichwa.!” Aliongea kirafiki huku anatabasamu na kunipa mkono.



    “hello Sarah.!” Nikampa mkono.



    Kwa namana ambavyo tulisalimiana mtu asiyetufahamu angeliweza kuhisi labda mimi na Sarah ni marafiki tulioshibana na labda hata siku nzima leo tulishinda wote kutokana na ureja reja wa namna ambavyo tulisalimiana. Lakini kwa mimi ambaye nilikuwa namfahamu Sarah vizuri nilikuwa bado najiuliza kichwani lengo la maigizo yote haya ya Sarah ilikuwa ni nini.



    Giselle alikuwa ametukata jicho fulani hivi mimi na Sarah tulipokuwa tunasalimiana. Tungekuwa katika mazingira mengine, siku nyingine toauti na hii siku ya leo ningeweza kuhisi lilikuwa ni jicho la wivu. Tulipokutanisha macho, Giselle aligeukia pembeni kuna kitu fulani ambacho sikukisikia akamueleza mwenzake Ilana.



    Japokuwa hii ilikuwa ni mara yangu ya nne kumuona Ilana, lakini hii ndio ilikuwa kama mara ya kwanza kumuona kutokana na mazingira yote ya awali nilipokuwa namuona kila mmoja wetu alikuwa anajitahidi kujifanya kuonyesha hamuoni mwenzake.



    Kwa hiyo leo ndio nilikuwa nimepata fursa nzuri zaidi ya kumtazama tena na kuzingatia mwanga angavu wa hii sebule ya kifahari tofauti na kule gizani ambako tulikuwa dakika chache zilizopita. Alikuwa ni binti mrembo haswa mwenye ngozi ya rangi ya maji ya kunde na uso mwembamba wa kitusi. Mrefu wa wastani na mwenye umbile zuri la saizi ya kati ambalo si kubwa sana na wala halikuwa dogo. Suruali yake ya suti na shati lake alilovalia vilimkaa sawa sawa na kuongeza uzuri zaidi ambao alikuwa nao.



    Kuna kitu ambacho tulipokuwa gizani nilishindwa kuking’amua kutokana na giza lakini hapa kwenye mwanga wa kutosha nikiwa naendelea kumuangalia moja kwa moja macho yangu yalitua mikononi mwa Giselle. Hakuwa na pete ya ndoa tofauti na ambavyo inapaswa kuwa. Wasi wasi wangu juu ya Giselle ulizi kuongezeka. Kwanza kushindwa kutambua tatizo lililosababisha mwenzake kushindwa kupumua, kisha kuogopa damu na sasa hana pete ya ndoa.



    Nilijikaza kiume ili yeyote kati yetu tuliopo pale asiweze kuhisi kilichokuwa kinaendelea kichwani mwangu.







    “The Prime Minister is going to be with you guys in a few minutes.!” Sarah aliongea kwa tabasamu huku anaondoka pale sebuleni.







    Moyo ulianza kunienda mbio kila ambavyo dakika zilivyokuwa zinakaribia kabla ya Waziri Mkuu kuja kuonana nasi. Sikuwa namuhofia Waziri Mkuu bali nilikuwa napatwa na wasi wasi kwamba kuna kitu hapa hakiko sawa na mbaya zaidi sikujua ni kitu gani. Si tu kwamba moyo ulikuwa unanienda mbio bali pia ulikuwa unauma, unauma kwa uchungu wa kila nilipofikiria kwamba kuna kitu hakiko sawa. Nikikumbuka kwa namna ambavyo kwa miaka miwili iliyopita nimepigana kufa na kupona, nimeishi maisha ambayo ni kama nillipita jehanum, yote hii ili kufanikisha kikao hiki, kikao cha siku hii ya leo, kikao kati yangu, Citibank na LE BLOC. Hii ni siku ambayo nahitaji kila kitu kiende sawa, ni siku ambayo hakutakiwi kuwa hata na chembe ya kukosea, ni siku ambayo itaamua sio hatma yangu tu, bali pia familia yangu kwa maana ya mke wangu Cheupe, mwanangu na mama yangu mzazi.







    Tukasikia ule mlango wa mbele unafunguliwa na na msafara wa watu ukaingia. Ulikuwa ni msafara wa Waziri Mkuu na walinzi wake karibia nane. Jambo ambalo mra moja lilinishitua ni kitendo cha Waziri Mkuu kuongozanana na walinzi wengi hivi. Wakati tunaingia hapa kichwani mwangu nilikuwa na uhakika kuwa Waziri Mkuu alikuwa kwenye lile jengo lingine la ofisi akimalizia shughuli zake. Na sio tu kwamba nilihisi, bali siku nzima ya leo nilikuwa nafuatilia mwenendo wa kila mahala ambapo Waziri mkuu alikuwepo na saa moja iliyopita nilikuwa nimehakikisha bila shaka yoyote kuwa Waziri Mkuu alikuwa ndani ya haya makazi yake.







    Lakini kitendo cha kuongozana na walinzi wengi hivi hii ilimaanisha kuwa alikuwa nje na haya makazi na muda huu ndio alikuwa narejea. Na hii ilikuwa inafafanua kwanini wakati tulipoingia mara moja niling’amua kuwa mahala hapa ulinzi ulikuwa ni mwepesi tofauti na ambavyo niilitarajia iwe. Sasa nilielewa kumbe sababu ilikuwa ni kutokuwepo kwa Waziri Mkuu muda huo tunawasili. Akili ilizidi kuvurugika, hii inawezekana vipi? Muda mchache uliopita kama saa moja tu iliyopita nilikuwa nimehaikisha kwa asilimia mia moja kwamba Waziri Mkuu alikuwa ndani ya Makazi yake hapa Mlimwa.







    Nikatupa jicho ukutani kwenye saa, ilikuwa ni saa tano na dakika kumi usiku. Ghafla moyo ulinipasuka na nikaanza kuhisi kijasho kwa mbali kinaanza kunitioka, nilianza kuelewa kwa mbali ni nini kilikuwa kinaendelea nyuma ya paza hapa. Nikaelewa kwa nini muda ule porini kabla hatujaondoka Giselle alitazama muda kwenye saa ya mkononi.







    “Habari yako kichwa.!” Waziri Mkuu Zephania Zuberi, ambaye mpaka siku tatu tu zilizopita alikuwa labda ndiye adui yangu namba moja juu ya uso wa dunia alinisalimia kwa bashasha huku anaketi kwenye sofa mbele yetu.











    WIKI MOJA ILIYOPITA – DODOMA HOTEL









    Imepita miaka mitatu, miezi minne, wiki mbili, siku sita, masaa kumi na nne na dakika ishirini na tano tangu siku ambayo nilimshuhudia baba yangu mzazi akielekeza bunduki kichwani mwake na kujipiga risasi mbele ya macho yangu. Siku hii sio tu kwamba ilikuwa ya ajabu kutokana na kitu ambacho baba yangu alikifanya mbele yangu, bali pia ilikuwa siku ya ajabu Kutokana na kuwa ndio siku yangu ya kwanza na siku ya mwisho kuwahi kumuona baba yangu mzazi. Sikuwahi kumpenda baba yangu wala kumchukia lakini kwa namna moja au nyingine tukio lile lilinifanya nikose ujasiri wa kuweza kukanyaga tena mji wa Dodoma kwa mika mitatu iliyopita mpaka siku hii ya leo.



    Kuna msemo ambao wanasema kwamba huwezi kamwe kuikimbia hatma yako, na hiki ndicho ambacho nilikuwa nahisi kilikuwa kimenitokea mpaka leo hii kujikuta niko tena kwenye mji ule ule ambao nilijiapiza kwamba sitakuja kukanyaga tena mguu wangu kwa maisha yangu yote yaliyobaki.







    Muda huu nilikuw nimekaa mahala fulani ndani ya hotel sehemu yenye mgahawa pembeni ya bwawa la kuogelea nakunywa kinywaji changu huku naangalia ile picha kwenye simu ambayo Issack alikuwa amenitumia ikiwa na maelezo yake.







    Wale mabinti wawili, mmoja wa Kiswahili japo nilihisi kabisa kwa muonekano wake lazima atakuwa Mnyarwanda na mwenzake wa kizungu walikuwa wanaendelea kufurahi pale kwenye bwawa la kuogelea huku wanajipiga ‘selfie’ kwa simu zao. Hii ilikuwa ni mara ya tatu naonana na mabinti hawa kwa ‘bahati mbaya’ na kila nikonana nao walikuwa wako na furaha hii hii huku wanapiga ‘selfie’. Lakini kutokana na maisha niliyopitia kwa miaka mitatu iliyopita nilikuwa na uwezo mzuri sana wa kung’amua kusudi la mtu hata kama alikuwa anajitahidi sana kulificha. Hii ilinifanya nijue kwa mara zote mbili mabinti hawa nilizokutana nao wakipiga ‘selfie’ uhalisia ni kwamba walikuwa wananipiga mimi picha. Hii ndio sababu ya kunifanya na mimi nitumie ‘uhuni’ wangu niliojifunza miaka yote hii mitatu kumpiga picha kwa siri yule binti wa Kinyarwanda na kumtumia Issack ili aone kama anaweza kufanya utundu wake wa TEHAMA na kujua yule binti ni nani.







    Muda huu ndio alikuwa amenitumia picha kadhaa za binti huyu ikiwa na maelezo machache tu ya msingi.



    “Giselle Jean Pierre



    27 years old



    Rwandan



    LE BLOC Agent”





    Maelezo haya machache yalinitosha kufahamu ni nini kilikuwa kinaendelea. Na niling’amua wazi kwamba kama huyu binti wa Kinyarwanda ni wakala wa LE BLOC basi lazima huyu binti wa kizungu atakuwa ni mtu wa Citibank.



    Kilichokuwa kinanichanganya ilikuwa ni kwanini walikuwa wananifuatilia kwa siri na walikuwa hawajitambulishi kwangu ?







    Nikapiga tena funda lingine la kinywaji changu na kisha kupiga simu kwenda kwa swahiba wangu Eric Kaburu ambaye mara ya mwisho tuliongea asubuhi ya siku ya leo.







    “Kichwa… habari yako?” Kaburu alinisalimia baada ya kupokea simu.







    “Nataka uandae kile kikao na Waziri Mkuu” nikaongea moja kwa moja hoja yangu bila kujibu salamu yake.







    Ukapita kama ukimya wa dakika moja nzima bila yeyote kuzungumza.







    “Ray.! Are you sure about this?”







    “I don’t know! Ila andaa kikao, kiwe wiki ijayo.!”







    “Citibank na LE BLOC wameshafika?”







    “Still not sure about that too!”







    “Una maana gani?”







    “Inawezekana wameshafika na niko nao hapa na inawezekana bado hawajafika”







    “Ray hivi hauwezagi kuongea vitu kwa lugha nyepesi bila mafumbo?” kaburu akafoka kwa kukereka.







    “Eric! Andaa kikao.!”







    “Ok boss.!” Akanijbu kwa kifupi.







    Nikakata simu.







    Nilijua fika kwanini Kaburu alikuwa anahofia kikao hikli nilichokipigania kwa zaidi ya miaka miwili sasa kati yangu, Waziri Mkuu, LE BLOC na Citibank.



    Alikuwa hawahofii Citibank au LE BLOC bali alikuwa anamuhofia Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, ambaye mpaka sasa alikuwa ndiye adui yangu namba moja chini ya uso wa jua.







    Labda ni ville tu sababu watu wengine akiwemo Kaburu pia, hajaishi maisha mabayo nimeyaishi kwa miaka mitatu iliypita. Safari hiyo ya maisha yangu mapya ambayo ilianza baada ya kwenda Zurich kwenye bank ambayo nilielekezwa na nayaraka nilizokabidhiwa na marehemu babab yangu. Safari ambayo ilinifanya nione upande wa pili wa siri wa maisha ya watawala na mifumo yake. Safari ambayo ilinifanya niielewe dunia katika namna ambayo wengi walikuwa hawaifahamu.



    http://pseudepigraphas.blogspot.com/



    Ni katika safari yangu hii ya Zurich na kutokana na mambo na vitu nilivyo viona na kukutana navyo huko ndio ilinifanya nijiapie na kujiwekea kanuni TATU za kuongoza maisha yangu tangu siku hiyo. Three Rules.



    Na kanuni ya kwanza, Rule number one; nilijiapia siku hiyo, tofauti na wengi wananvyo amini na kuaminishwa ila mimi niliamini kwamba… katika maisha hakuna rafiki wa kudumu, hakuna adui wa kudumu, na wala hakuna maslahi ya kudumu. There is only survival.







    Na hii ndio sababu iliyokuwa inanifanya intake kikao na adui yangu Waziri Mkuu wa Jamuhuri, Zephania Zuberi.







    Nikapiga fundo la mwisho la kinywaji changu, na kisha nikainuka kuelekea juu ghorofani pale hotelini kilipo chumba changu nilichofikia.







    Simu ya Cheupe bado ilikuwa inaita bila kupokelewa kwa karibia mara ya tano sasa niliyojaribu kupiga. Sikujua bado ni kwa sababu gani simu ilikuwa haipokelewi japo moyoni bado nilikuwa na hisia mbaya kuhusu kilichokuwa kinaendelea, lakini niliendelea kujipa moyo kwamba kila kitu kiko sawa.



    Nikainua tena simu na kubofya kumpigia Issack,







    “Niaje kichwa?” Issack alinisalimu mara tu baada ya kupokea simu







    “Poa poa… uko wapi?”







    “Ofisi kwangu.”







    “naomba uende forest home ukamcheki shemeji yako..!”







    “kuna tatizo kwani?”







    “sijajua ila simu yake haipokelewi tangu mchana…”







    “Poa mkuu dakika sifuri tu nakupa jibu..!”







    “Thanks!”







    Nikakata simu.











    Nilikuwa naongea na simu huku nimesimama kwenye dirisha la chumba changu cha hotel naangalia nje kwenye bwawa la kuogelea.



    Chumba changu cha hoteli kilikuwa kiko katika usawa ambao kutoka dirishani uklikuwa unaweza kabisa kuona sawia bwawa la kuogelea na mgahawa ulio pembeni yake. Nilikuwa nimegundua kwamba wale mabinti wawili, yule wa kizungu na mwenzake mwenye muonekano kama mnyarwanda walikuwa wanapenda kutumia muda wao bwawani pale au kwenye mgahawa kila siku muda wa asubuhi na jioni. Lakini ajabu ni kwamba leo sikuweza kuwaona na wala hakukuwa na dalili yeyeote ya uwepo wao.







    Nilikaa kwa dakika kumi nzima dirishani nikichungulia labda wangeweza kutokea muda wowote lakini hakukuwa na mafaniko yoyote yale.



    Ghafla nikasikia mlango unagongwa.







    “nani?” nikauliza kwa tahadhali.



    “Muhudumu.!” Sauti ikanijibu upande wa mlango.











    Nikafungua mlango haraka.







    “habari za jioni.!” Muhudumu wa kike alinisalimu akiwa amesimama mbele ya mlango wangu baada kufungua.







    “poa kabisa..”







    “kuna mzigo wako huu umeachwa pale mapokezi..!” muhudumu alinieleza huku ananipatia bahasha.







    “ni nani ameuleta?” nikauliza nikiwa napokea bahasha na kuanza kuifungua.







    “hakuacha jina… alisema ni mzigo wako unautegemea kwa hiyo utaelewa.!”







    “asante sana!” nikashukuru huku naanza kufungua bahasha.







    Nilifungua bahasha kwa haraka na ndani yake kulikuwa na kipande cha karatasi cha ukubwa wa wastani. Nilipoitazama karatasi hii ambayo ilikuwa na maneno kadhaa laki ni kwa haraka sana jicho langu lilitua kwenye neno “December 19”.







    “Dada.! Samahanii..” nilimuita muhudumu ambaye tayari alikuwa amefika hatua kadhaa kutoka mlangoni akiwa anaondoka.







    “bila samahani..!” alinijibu huku anarejea tena pale mlangozi kwangu.







    Kunajambo nilikuwa nataka kumuuliza lakini kwa namna ambayo nilimsoma haiba yake kwa haraka nilijua kabisa hawezi kunieleza kwa kuzingatia maadili yake ya kazi. Wanasema kwenye udhia penyeza rupia. Ndicho nilichokifanya, nikaingiza mkono mfukoni na kutoa noti kadhaa za fedha, nikachomoa noti mbili za elfu kumi kumi na nyingine nikazirudisha tena mfukoni.







    “samahani nilikuwa sijakushukuru..!” niliongea huku namkabidhi zile noti mbili za shilingi elfu kumi kumi.







    “Usijali.! Asante sana kaka..” alipokea huku anatabasamu karibu meno yote yako nje.







    “kuna jambo nahitaji unisaidie kidogo kama hutojali..!”







    “jambo gani kaka?” aliuliza kwa wasi wasi. Kawa akili ya haraka haraka niliweza kumsoma kuwa alikuwa anahisi labda nataka kuongea masuala ya mapenzi.







    Ilibidi niende kwenye hoja yangu haraka ili kuepusha hisia niliyomuona ameanza kuipata kichwani.







    “kuna wageni wenu wawili mabinti.. mmoja ni mzungu na mwenzake mweusi… unaweza kujua kama wapo au wameshaondoka?” nilimuuliza kwa reja reja tu bila kuwa na uso ‘serious’. Nia yangu nilikuwa nataka apate hisia labda nilikuwa namtaka kimapenzi mmojawapo wa hao ninao waulizia.







    “mmmh! Ngoja nicheki nitakuja kukushtua.” Yule muhudumu alijibu huku anatabasamu.



    “pamoja na hilo naomba uangalie na kunipatia majina yao kamili waliyo andikisha hapa, wanakotoka na taarifa nyingine ambazo wameandikisha.!”







    Nilipoongea haya nilimuona uso wake unabadilika kutoka kwenye tabasamu na kuwa uso wa ‘kazi’. Nadhani sasa alijua kuwa sikuwa na nia ya kimapenzi juu ya haoa mabao nawaulizia bali lilikuwa suala lingine kabisa ambalo linaweza kuwa muhimu au la hatari. Sikutaka hisia hii ikue ndani ya kichwa chake, kwa hiyo ilinibidi nifanye kitu haraka ili kumlainisha tena. Nikaingiza tena mkono mfukoni na kutoa noti nyingine mbili za elfu kumi kumi.







    “hii utaongezea hapo ya vocha.!” Nikamshikisha mkononi huku amenikazia macho bila kuangalia pale mkononi ninako mpa fedha kama vile alikuwa hataki. Ilibidi nimfunue kiganja cha mkono, niweke hela alafu nimkunje tena kiganja.







    Tuliangaliana kwa sekunde kadhaa kisha akageuka na kuondoka pasipo kusema kitu chochote kile. Moyoni nilikuwa naomba dua kimya kimya afanye kile ambacho nimemuomba, anisaidie kupata taarifa za wale mabinti wawili, mzungu na mwenzake mweusi. Nikafunga mlango na kuingia tena ndani chumbani.



    Macho yangu yalikuwa yametua tena kwenye simu ambayo niliiacha kitandani, niliangalia kama kuna meseji au walau simu iliyopigwa, na sio simu tu bali simu kutoka kwa mkewangu Cheupe. Bado hakukuwa na chochote.







    Nikainua simu na kupiga tena namba ya Cheupe. Safari hii ilikuwa haipatikani kabisa. Moyo ulinienda mbio zaidi nikimuomba Mungu nipate jibu la haraka kutoka kwa Godi niliyemtuma aende nyumbani.







    Nikarejea tena kusoma ujumbe ulioandikwakwenye kile kijikaratasi kilicholetwa kwenye bahasha na muhudumu. Nikakisoma tena na tena kuhakikisha kuwa nilichokuwa nakielewa kilikuwa ni sahihi na hakukuwa na chochote ambacho kilikuwa kinanipita. Ujumbe wenyewe ulikuwa ni mfupi tu lakini kama nilikuwa nimeuelewa kwa usahihi ulikuwa na maana kubwa sana.











    “DECEMBER 19







    7712/LH. A+. A+







    CITIBANK. ZURICH.”











    Nilielewa huu ujumbe ulikuwa na maana gani, lakini kilichoniumiza kichwa nilikuwa najiuliza ni nani aliacha mapokezi na kutaka uletetwe kwangu? Kwa asilimia kubwa sana nilihisi kwamba ni wale mabinti wawili ndio waliokuwa wananifanyia huu mchezo. Lengo lao na dhamira yao haswa bado sikuijua. Nikasogea tenba dirishani na kuanza kuchungulia bwawani na kwenye mgahawa moyoni nikiwa na tumaini dogo labda nitawaona tena wale mabinti. Nilisimama pale dirishani kwa takribani dakika kumi kichwa kikiwa kinawaka moto haswa nisijue ni wazo lipi nilipe nafasi ya kulichakata kwenye ubongo.



    Kwa upande mmoja bado nilikuwa kwenye kitendawili cha kwa nini simu ya Cheupe ilikuwa haipokelewi na sasa hivi ilikuwa haipatikani kabisa. Upande mwingine nilikuwa najiuliza kwa nini hawa mabinti walikuwa wananifuatilia kwa siri ingawa kama nilikuwa sahihi moyoni mwangu niliamini kwamba wametumwa hapa ili kuja kuonana na mimi, lakini ajabu walikuwa hawajajitambulisha kwangu, kitu pekee walichokuwa wanakifanya ni kufuatilia nyendo zangu kwa siri kubwa.



    Upande mwingine nilikuwa kwenye kitendawili cha huu ujumbe nilioletewa kwenye bahasha dakika chache zilizopita. Ujumbe wenyewe haukuwa kitendawili kwangu, bali swali lililo niumiza kichwa lilikuwa ni nani alikuwa ameleta ujumbe huo. Jibu rahisi zaidi la swali hili lilikuwa ni wale mabinti wawili. Lakini sikujua kwa nini kuna upande fulani wa moyo wangu ulikuwa unakataa jibu hili.







    Nikaona hakukuwa na haja ya kuendelea kuumiza kichwa wakati kulikuwa na njia rahisi zaidi ya kupata ukweli.



    Nikafunga mlango wa chumba changu na kuteremka mpaka chini mapokezi ya hoteli. Pale mapokezi niliwakuta wadada wawili lakini yule dada ambaye aliniletea bahasha juu chumbani kwangu hakuwepo tofauti na nilivyodhani kwamba atakuwa ni dada wa hapa mapokezi.







    “habari zenu waerembo!”







    “nzuri tu kaka!” wakaniitikia kwa pamoja kwa tbasamu.







    “nililetewa bahasha juu chumbani kwangu… nilikuwa na uliza ni nani ambaye aliicha bahasha hiyo hapa na kusema iletwe kwangu?” nikawauliza.







    Wale wadada walionekana kushanga kana kwamba walikuwa hawajui ni nini nilikuwa naongea.







    “bahasha gani kaka?” mmoja wao akaniuliza kwa mshangao kidogo.







    “bahasha nimeletewa na muhudumu mmoja kati yenu japo sio nyinyi.. ameniletea juu chumbani dakika chache zilizopita.





    Nikajieleza tena huku na mimi nawashangaa wao kwa kutokujua ninchowauliza.











    “kwa kweli sifahamu hicho kitu kaka.. hatujapokea bahasha yeyote hapa siku ya leo.!” Dada mmoja wapo akanijibu akiwa na uhakika na anachokiongea huku pia akiendelea kunishangaa kwa nianchoiuliza.







    “una uhakika kuwa hamjapokeaa bahasha hapa siku ya leo?” nikamuuliza kwa udadisi zaidi muda huu nilianza kupata wasiwasi moyoni.







    “nina uhakika kaka.. hatujapokea bahasha yeyote hapa mapokezi siku ya leo! Ni nani ambaye alikuletea hiyo bahasha?” akaniuliza.







    Nikaanza kuwaelekeza muonekano wa huyo muhudumu aliyeniletea bahasha na muda gani hasa aliniletea.







    “atakuwa ni Siwatu huyo!” yule muhudumu mwingine akadakia nikiwa bado naendelea kuwaelekeza muonekano wa huyo muhudumu ambaye aliniletea bahasha.







    “hebu kamuite aje aeleze!” muhudumu wa kwanza yule ambaye alionekana kama kwa namna fulani alikuwa ni kiongozi wa wenzake au wanamuheshimu kwa namna fulani aliongea huku anamuagiza mwenzake ili “Siwatu” akaitwe.











    Kama dakika tano baadae yule muhudumu alirejea akiwa na muhudumu mwingine ambaye ndiye alikuwa ni yule aliyeniletea bahasha juu chumbani kwangu.





    “yani huyu Siwatu hata hasikii.. yani ana mambo ya kijinga sana huyu” yule muhudumu alikuwa anakuja anafoka na mwenzake ambaye sasa nilimfahamu kuwa alikuwa anaitwa Siwatu, yule ambaye aliniletea bahasha.







    “nini tena?” yule uhudumu niliyebaki naye pale mapokezi aliuliza huku anasimama.







    “hebu msikie anachokisema!” yule mwenzake aliongea tena kwa kufoka.







    Walifika mpale mapokezi huku wote macho tukiwa tumemkodolea Siwatu. Siwatu mwenyewe alikuwa amejikunyata kwa woga ana angalia chini.



    Sasa hivi ndio niligundua tofauti ya sare alizovaa Siwatu na sare ambazo walikuwa wamevaa wale wadada wa pale mapokezi. Siwatu alikuwa amevaa shati na suruali ya kitambaa rangi ya bluu-nyeusi. Wale dada wa pale mapokezi mmoja alivaa suruali na mwingine sketi fupi lakini zote za rangi kama ya sare za Siwatu lakini wao walivalia na mashati meupe juu.







    Kwa uzoefu wangu wa kukaa mahotelini niligundua mara moja kuwa Siwatu alikuwa ni muhudumu wa masuala ya usafi vyumbani kwenye hii hoteli.







    “hebu nielezeni, nini?” yule muhudumu niliyebaki naye pale mapokezi aliongea kwa sauti ya taratibu safari hii.







    “samahani dada nilijisahau nikapokea mzigo kutoko nje!” Siwatu alijieleza huku ameanzgalia chini alafu anabinya binya vidole kwa uoga.







    “wewe Siwatu utazoea lini kazi jamani?? Mara ngapi nakueleza usipokee mizigo huko nje… ukipewa bomu je?” dada wa pale mapokezi alifoka.







    Niliwaelewa ni nini walikuwa wanakiongelea. Inaonekana kuwa aliyeleta bahasha ile hakuingia ndani ya hoteli hapa mapokezi, bali kwa namna fulani alimkabidhi mzigo Siwatu wakiwa nje ya Hoteli.







    “ok! Hakuna shida ilikuwaje kwani dada’ngu?” nikauliza huku nikiwatuliza wale wenzake wasiendelee kuofoka.







    “nilikuwa nadeki hapo nje kwenye korido ndio kuna mkaka akaja na gari akasimamisha akanipa ile bahasha akanieleza kuwa nikuletee chumbani kwako… nilipomuuliza nikwambie imetoka wapi, akanijibu kwamba ameandika humo ndani na wewe unajua.!” Siwatu aliongeaa huku amejiinamia chini anabinya binya vidole mikononi.







    “umamkumbuka muonekano wake?” nikamuuliza tena.







    “mweupe hivi alafu ana mandevu mengi amenyoa ‘timbalendi’.” Siwatu aliongea huku bado amejiinamia.







    Mara moja nikaelewa ni nani alikuwa ameleta bahasha hiyo. Alikuwa ni Godfrey au Godi kama ambavyo tulipendelea kumuita. Nikajitahidi nisionyeshe mshtuko wangu.







    “msijali nimeshafahamu ni nani ameleta huu mzigo… ni rafiki yangu! Msijali..” nikaongea kwa kujiamini huku nikiwatuliza wasiendelee kufokeana.







    “hapana kaka… huyu hasikii… hapa hotelini yanatokea mambo mengi… mtu akileta mzigo wa mteja ili apelekewe chumbani huwa tunataka akabidhi hapa mapokezi sio kupeana kienyeji hivyo… mfano huo mzigo ukipotea tunafanyaje? Nani atawajibishwa… Siwatu hili sula lisitokee tena la sivyo namfikishia boss hii taarifa..!!” dada wa mapokezi pale akafoka.







    “yani huyu mzito sana kuelewa.. wiki nzima hii bado tu haujajua maadili ya kazi yako? Mwenzake naye akaongezea.







    Aliposema hili neon “wiki nzima” nilijikuta kama kuna taa fulani hivi imewaka kichwani mwangu. Kuna hisia fulani hivi nikaipata kana kwamba kuna jambo fulani hapa la zaidi natakiwa kulijua. Nahisi Siwatu naye kwa namna fulani neno hili lilikuwa limemgusa maana nikamuona amenikata jicho fulani hivi la kuibia ibia nisigundue kuwa ananiangalia.







    “basi limeisha hili jamani kuweni na amani… Siwatu usisahau ile kazi niliyokutuma uifanye sawa?” nikaongea huku naanza kutembea kuelekea mlango wa kutokanje ya hoteli.







    “Sawa kaka!” siwatu akanijibu kwa heshima zote.







    Nikafungua mlango na kutoka nje. Nyuma yangu nikasikia wenzake wanamuuliza, “kazi gani amekutuma?” alafu nikmsikia Siwatu anawajibu, “kuna nguo chumbani kwake anataka zipigwe pasi.”







    Nikajikuta natabasamu na ucheka namna ambavyo Siwatu aliweza kutunga uongo wa haraka haraka namna ile. Kazi niliyokuwa namkumbushia kuifanya ilikuwa ni kunipatia taarifa za wale mabinti mzungu na mwenzake mnyarwanda, lakini alijiongeza akili haraka haraka na kuwaeleza wenzake kuw





    kuwa nimemtuma kunipigia pasi nguo.



    Bado kuna kitu fulani kichwani nilikuwa nashindwa kukichakata kuhusu Siwatu, hasa hasa baada ya mwenzake kutamka kauli ya “wiki nzima hii bado tu hauelewi kazi”… japo ilikuwa kauli ya kawaida tu lakini ilikuwa inaninyima raha ndani ya nafsi. Ina maana Siwatu amekuwa kazini pale kwa wiki moja tu? Sikuelewa ni kwanni lakini nafsi yangu ilikuwa haijatulia kuhus suala hili.







    Lakini pia nilikuwa najiuliza kuhus Godi kumpa Siwatu kikaratasi kile. Godi alikuwa amepata wapi kile alichoandika. Jibu zuri ambalo lilikuja kichwani ilikuwa ni kwamba Godi alikuwa ameagizwa na mtu aniletee ile bahasha. Lakini kwanini asinipigie simu kunieleza kuwa ana mzigo wangu ili anikabidhi mwenyewe badala yake anauacha mapokezi tena bila maelezo ya kujitosheleza? Nikahisi labda atakuwa alikuwa na haraka mno.







    Nikavuka barabara na kwenda mpaka upande wa pili ambapo kuna kibanda cha chips kinaangaliana na hoteli na nikakaa hapo. Nikaagiza mishikaki tupu na soda na kuanza kula taratibu huku natafakari vitendawili ambavyo vilikuwa kichwani mwangu. Kwa kiasi fulani kichwa kilikuwa kinakaribia kupasuka nikijitahidi kufikiri japo niweze kung’amua machache kati ya yale ambayo yako kichwani mwangu.







    Nikiwa bado nandelea kula mishikaki yangu nikisindikiza na kinywaji, mara simu yangu ya mkononi iliita.







    “Issack… nipe ripoti.” Nilipokea simu.







    “Kichwa tafadhali naomba urudi Morogoro leo!” Issack aliongea kwa sauti ya woga lakini iliyo makini.







    Nilijikuta moyo umepasuka, pwaaa.!







    “kuna nini Issack… mke wangu na mwanagu wako salama?” niliuliza huku nimeanza kuhema kwa woga wa kupokea habari mbaya.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/





    “Kichwa!! Naomba urudi Morogoro sasa hivi… yani hivi ninavyoongea nataka uwe unakusanya vitu vyako unaanza safari!” Issack alionngea kwa sauti ya kufoka safari hii baada ya kuona simsikilizi anachonisisiotiza.







    “ok ok ok! Calm down Issack… najiandaa sasa hivi nirudi, lakini naomba unieleze walau moyo wangu utulie… mkewangu na mwanagu wako salama?”







    “wako salama… tuko nao hapa mimi na Godi”







    Nilihisi kama dunia imepasuka. Godi?? Godi anawezaje kuwa Morogoro muda huu? Kwa maelezo ya Siwatu japo hakutaja jina lakini ni dhahiri kuwa aliyekuwa anamuongelea alikuwa ni Godi.







    “umesema mko na Godi hapo?” nikauliza kwa sauti ya chini lakini iliyo thabiti.







    “kichwa rudi Morogoro sasa hivi kuna situation hapa.. yes, niko na Godi, mkeo na mwanao Ayanda!” Issack akafoka tena.







    Nikajikuta nimekata simu bila kujibu chochote kile. Nikakumbuka ile kauli ya yule muhudumu, “wiki nzima sasa bado tu hujaelewa kazi.” Ina maana Siwatu ana wiki moja tu tangu aanze kazi pale Dodoma Hoteli? Taa ikawaka tena kichwani mwangu. Kuna mchezo hapa ulikuwa unafanywa na huyu anayejiita Siwatu.







    Sikumbuki kama nilimlipa mwenye chips au ni muda gani nilivuka barabara kurejea upande wa hoteli, ninachokumbuka ni namna ambavyo nilikuwa natembea haraka na kwa hasira kuelekea mapokezi ya hoteli.







    “Siwatu yuko wapi?” niliuliza huku nahema baada ya kufika mapokezi.







    “uko sawa kaka?” dada wa mapokezi mmoja wa wale niliowakuta mara ya kwanza aliniuliza kwa mshangao huku akiwa na woga kutokana na uso wangu wa hasira.







    “Siwatu yuko wapi?” niliuliza tena kama sijasikia swali lake.







    “ameondoka nyumbani shift yake imeisha.!!” Dada alinijibu huku amenitumbulia macho kwa woga.







    “fuuucck!” tusi lilinitoka bila kujijua na haraka nikaanza kupanda ngazi kuelekea juu chumbani kwangu.







    Nilielewa kuwa huyu anayejiita Siwatu hawezi kurudi tena hapa hata hiyo kesho. Alikuwa hapa kwa kazi maalumuna kazi hiyo alikuwa amesha itekeleza. Tatizo nilikuwa bado sijajua ni kazi gani hasa. Kunipatia ile bahasha? Lakini mbona kila kilichoandikwa ndani yake japo ni siri kubwa lakini havikuwa vipya kwangu. Labda tu ni kitendawili kingine cha kujiuliza ni namna gani alikuwa amepata ile taarifa maana ni watu wachache mno tunaofahamu kitu hicho. Mimi, marehemu baba yangu na Rais wa bank ya Citibank.







    Sikutaka kupoteza muda zaidi, kwa usalama wangu natakiwa kuondoka hapa mkara moja kabla jambo baya halijatokea. Nilikuwa tayari nimefika mbele ya mlango wa chumba changu. Nilitoa funguo haraka haraka mfukoni na kufungua mlango.







    Nilipofungua tu mlango kitu cha kwanza nilichokiona ilikuwa ni bahasha kubwa kama size ya A4 ikiwa sakafuni. Nikashituka.



    Nikainama kuikota. Juu ya bahasha kulikuwa na maneno, “Kazi uliyonituma” yameandikwa kwa kalamu ya wino. Nikaanza kuifungua huku moyo unaenda mbio na kijasho chembamba kinachuruzika.







    Nilipofungua ndani ya bahasha nilikuta picha ya wale mabinti wawili, mzungu na yule mnyarwanda. Pamoja na hizo picha kulikuwa na kama karatasi nne zilizochapwa maandishi mengi sana ambayo japo sikuyasoma kwa muda huo lakini yalionekana kuwahusu wale mabinti.



    Kama nusu saa iliyopita nilimuomba Siwatu anipe taarifa za wale mabinti wawili ambazo waliziandikisha hapa hotelini, but this was too much. Taarifa hizi zimetoka au amezitoa sehemu fulani adhimu, hoteli abadani hawawezi kuwa na taarifa kama hizi.







    Nikajikuta najiuliza swali kichwani ambalo nilipaswa kujiuliza muda wote huu, “HUYU SIWATU NI NANI? NA ANATAKA NINI?”







    Mara simu yangu ya mkononi ikaita, nikatupa jicho kwenye kioo, jina lilisomeka, “ERIC KABURU”.







    Mapigo ya moyo yakaongezeka maradufu. Nilihisi mpaka kizunguzungu.







    Sikujua kwanini lakini nilijikuta nasita kupokea simu ya Kaburu. Nilibaki naitazama tu jinsi ambavyo ilikuwa inaita. Kichwani nilikuwa najiuliza hii ilikuwa bahati mbaya au kulikuwa na muunganiko kati ya simu ya kaburu na bahasha iliyo mkononi mwangu ambayo niliikuta pale sakafuni. Kuna wazo fulani kichwani lilikuwa linaniambia kuwa nisipokee ile simu ya Kaburu lakini pia upande mwingine kuna wazo lilkuwa linanijia kwamba hakukuwa na uhusiano wowote kati ya simu ya Kaburu na bahasha iliyo mkononi mkwangu.







    “haloo..” nilijikuta nimepokea simu bila kufikiri mara mbili mbili.







    “uko wapi Ray?” Kaburu aliniuliza bila hata kujibu salamu yangu.







    “bado niko Dodoma Eric…”







    “Nahitaji uje Dar leo hii kwa namna yoyote ile!” Kaburu aliongea kwa sauti ya chini kama vile kuna watu ambao alikuwa hataki wasikie anachozungumza.







    Nilijikuta nashindwa kuongea neno lolote. Kama kuna kitu ambacho nilikuwa natamani muda huu basi ilikuwa ni kutopata habari ambayo ingenIongezea kitendawili kingine kichwani mwangu. Kwa sauti hii na jinsi ambavyo Kaburu alikuwa anaongea ilikuwa ni dhahiri kabisa kwamba kulikuwa na kila dalili ya kichwa changu kuvurugika tena kutokana na habari mbaya nyingine ambayo ingeongeza sintofahamu ambyo tayari ilikuwa imenielemea kichwani.



    Nilifumba macho kwa nguvu na kutazama juu.







    “kuna nini Dar?” nikamuuliza huku bado nimefumba macho.







    “Ray nahitaji uje haraka iwezekanavyo… vitu vingine vyote nitakueleza huku… si sawa tukionge kwenye simu.” Aliongea kwa sauti ya kunong’ona zaidi safari hii.







    “Kaburu natakiwa pia niwe Morogoro leo hii kwa dharura maalumu… kwa hiyo ni vyema unieleze ni nini hasa ambacho kinaendelea huko Dar.!” Nikapngea kwa kufoka.







    “Nimeletewa ujembe kwenye bahasha ambao nadhani unakuhusu.!”







    Sikushituka kwa sababu ya kunieleza kuwa kuna ujumbe ameletewa, bali lilikuwa ni neno bahsha ndilo ambalo lilinishitua. Kuna muda unatamani kama uwezo kupotea na usiwepo kwenye maisha haya au kwenye dunia hii. Na kuna muda unatamani labda ubadilishane na mtu mwingine maisha yako. Ndivyo ambavyo nilikuwa najisikia muda huu. Japo bado nilikuwa sifahamu ujumbbe huo alioletewa ulikuwa unahusu nini lakini lakini tayari akili tyangu na kichwa changu kilikuwa kimevuruhika na nilikuwa sitamani kusikia zaidi. Sintofahamu ambayo ilikuwa kichwani mwangu ilikuwa imenielemea tayari, nilikuwa sihitaji sintofahmu nyoingine tena kichwani.







    “Ray.., bado hewani?” kabru aliongea. “Ray.. Ray..”







    “Niko hapa Eric.!” Nilijibu kwa sauti ya unyonge kabisa.







    “Unakuja ama vipi?”







    “Hiyo Bahasha ina ujmbe gani?” niliuza kwa sauti ya unyonge.







    “Sidhani kama ni sahihi kuongea hili kwenye simu!”







    ”Eric huo ujumbe unahusu nini?” nikamuuliza kwa hasira.







    “ok… ok.!! Umeandikwa ‘December 19, 7712/LH ZURICH, CITIBANK’..” Kaburu aliusoma ujumbe kwa taratibu.







    Niligundua kuwa kwenye ujumbe huu ambao Kaburu alikuwa ananisomea japo ulikuwa unafanana kabisa na ule ujumbe ambao nililetewa na Siwatu muda mfupi uliopita lakini ulikuwa hauna vitu kadhaa.







    “Umenisomea huo ujumbe kwa usahihi?” nikamuuliza.







    “Yes! Umeandikwa hivyo… ‘December 19, 7712/LH ZURICH, CITIBANK’..” akarudia tena kunisomea.







    Safari hii niliamini kuwa hakuwa amesahau kitu chochote kukisoma. Ujumbe ambao alikuwa amepelekewa ulikuwa tofauti na huu ambao nilikuwa nao ulioletwa kama lisaa limoja lililopita. Ujumbe wake huu alionisomea ulikuwa hauna neno ‘A+. A+’. pia katika ujumbe wangu neno ‘Citibank’ lilitangulia kabla ya neno ‘Zurich’ tofauti na ujumbe ambo Kaburu alinisomea, neno ‘Zurich’ lilikuwa limetangulia. Nilijua fika kwamba hii haikuwa bahati mbaya, yeyeyote ambaye alikuwa anajaribu kucheza na akili yangu alikuwa na maana kutofautisha jumbe hizi mbili.







    “Uliandaa kile kikao nilichokwambia?” nikamuuliza Kaburu.







    “Ray hivi umesikia kitu ambcho nimekueleza?” Kaburu aliongea kwa sauti ambayo japo niliku





    “Ray hivi umesikia kitu ambcho nimekueleza?” Kaburu aliongea kwa sauti ambayo japo nilikuwa simuoni lakini nilijua kuwa alikuwa kwenye mshangao.







    “Siwezi kuja Eric… andaa kikao na Waziri Mkuu!” niliongea kisha nikakata simu.







    Kuna mtu ameijua siri kubwa kuhusu mimi na likuwa anajaribu kunichezea akili. Sikujua lengo lake hasa lilikuwa ni lipi lakini ilionekana dhahri kuwa alikuwa na lengo mahususi kabisa kuhus hiki ambacho alikuwa anakifanya.







    Nikajirusha kitandani na kulala kuangalia juu ya dari. Nilhisi dunia yangu ilikuwa inataka kupasuka vipande vipande kabla hata azma yangu kutimia. Nikajaribu kuwaza na kuwazua. Ni nini ambacho kilikuwa kinaendelea? Ni nani ambaye alikuwa ananichezea akili?



    Niliwaza tena na tena kuhusu kuachwa kwa herufi A+,A+ kjatika ujube ambao Kaburu alikuwa amepelekewa. Kwa ambao tunafahamu suala hili na maana yake, ambao nilikuwa naamini tulikuwa watu watatu tu yaani mimi, marehemu baba yangu na Rais wa Citibank.. A+ ilikuwa inamaanisha kundi langu la damu.







    Miaka mitatu iliyopita, siku ya kwanza ambayo nilipelekwa kwenye ghorofa la PPF house waliponitoa damu na kuondoka nayoo sikuelewa walikuwa wanaifanyia nini. Ni mpaka siku ambayo nilifika Zurich ndipo ambapo nilielewa kwa nini wanachama wote wa jumuiya ya siri ya The Board walikuwa wanachukuliwa damu siku ya kwanza tu wanapojiunga na jumuiya hiyo.



    Kila ambavyo nilikuwa nafikiria kichwani nilikuwa nakosa jibu la kwanini herufi hizo zinazowakilisha kundi langu la damu, A+ zilikuwa zimeachwa katika ujumbe ambao kaburu alikuwa amepelekewa. Na ni nani hasa alikuwa anafanya mchezo huu?







    Kwa upande fulani nikaanza kuhisi labda kuna mtu au kikundi fulani cha watu ambacho kilikuwa kinajaribu kukwamisha juhudi zangu zilizonileta hapa Dodoma… nilianza kuhis labda kuna watu ambao walikuwa hawataki nifanikiwa kukamilisha kitu ambacho kilikuwa kimenileta hapa Dodoma. Na kama kuliuwa na mtu au watu ambao walikuwa hawataki nifanikiwe kukamilisha kilichonileta hapa ni nani au akina nani?







    Walau sasa kidgo nikaanza kuona kuna taa ilikuwa inawaka kichwani mwangu. Hili ndilo swali ambalo nilikuwa natakiwa kujiuliza muda wote huu. Ni nani ambaye anaweza kuwa na mslahi ya kutotaka kuona nilichokuja kukifanya hapa Dodoma kilikuwa hakifanikiwi.







    Ili niwe kwenye muelekeo sahihi wa kupata jibu la swali ambalo nilikuwa najiuliza kichwani nilikuwa napaswa kutembea hatua kwa hatua kichwani mwangu na kuhusu lengo langu hasa la kuwa hapa Dodoma.







    Nikaanza kuwaza kuanzia mwanzo kabisa wa dhamira yangu…







    Kutokana na safari yangu ya Zurich miaka miwili iliyopita, licha ya mambo mengi na siri nzito ambazo nilikutana nazo huko kutokana na kufuata maelezo niliyoyakuta kwenye nyaraka ambazo nilikabidhiwa na maraehemu baba yangu siku ambayo alijipiga risasi mbele yangu, nilijikuta kwa namna moja au nyingine nilichokiona zurich kilipandikiza kusudi la kimaisha ndani yangu, a purpose. Kusudi ambalo nisingeweza kumueleza mtu yeyote. Kusudi ambalo nisingeweza kulieleza kwa mtu akanielewa, kusudi ambalo lilikuwa ni vyema zaidi nikibaki nalo mwenyewe moyoni mwangu.







    Japokuwa nilijua dhahri kwamba kuna uwezekano mkubwa wa kuijenga tena upya jumuiya ya siri ya The Board ili niweze kutimiza kusudi hili, lakini sikuwa na jinsi nyingine ya kufanya.







    Swali ambalo sasa nilihisi nilikuwa napaswa kujiuliza, ni nani ambaye kwa namna yeyete ile asingekuwa tayari kuona dhumuni langu hili linafanikiwa? Au nikijiuliza swali mahususi zaid, ni nani ambaye asingependa kuona The Board inarejea tena kama akihis kuna mazingira ya jumuiya hiyo kuundwa upya?







    Jibu ambalo lilikuwa linaninjia kichwani nilikuwa sitaki kuliamini, nilihisi niendelee kutafakari labda nipata jibu mbadala. Lakini kila mbavyo nilikuwa natafakari zaidi nipate jibu mbadala ndivyo ambavyo nilikuwa nazidi kuona kichwani mwangu kuwa jibu ambalo nilikuwa nalo tayari ndilo ambalo lilikuwa jibu sahihi zaidi.







    Kwa namna ambavyo nimeishi miaka miwili iliyo pita au miaka mitatu kwa kuwa sahibhi zaidi, na kwa mambo ambayo niliyaona na siri ambazo nimefanikiwa kuzing’amua, ni





    The Bold: , nilkuwa na hakika bila shaka yeyote kichwani mwangu kuwa kama kuna mtu au watu ambao kwa gharama yeyote ile wasingeweza kukubali kuona The Board inarejea basi walikuwa ni Rais wa nchi na mke wangu mpenzi Cheupe.







    Kama ningemueleza mtu jibu hili nina amini kabisa anenihis labda nimechanganyikiwa. Lakini uhalisia ulikuwa ni kwamba hili ndilo jibu ambalo kichwani mwangu lilikuwa linaleta maana zaidi. Kama kuna mtu alikuwa anafanya huu mchezo basi alikuwa ni Rais wa nchi au mke wangu Cheupe.







    Nikainuka kitandani na kuchukua taulo kwenda bafuni. Nilidhamiria kuwa kwa namna yyote ile, ni lazima nitimize kilichonileta hapa Dodoma na kwa namna yeyeote ile lazima nifahamu ni nani yuko nyuma ya ii sintofahamu niliyokuwa nayo kichwani.







    Niliona huu ndio ulikuwa muda sahihi wa kuweka mtego ili walau nianze kupata mwanga wa sintofahamu ambayo nilikuwa nayo kichwani. Kabla sijaingiabafuni nilichukua simu na kuandika ujumbe mfupi.







    “Mueleze mke wangu kuwa sitaweza kurudi Moro leo..”







    Nikamtumia ujumbe huu Issack na kisha nikaingia bafuni.







    Nawezekana kuwa mwendawazimu kumtilia mashaka mkewangu, lakini baada ya safari yangu ya Zurich na vitu ambavyo niliviona huko. Nilijiwekea kanuni tatu za kuongoza maisha yangu. Kanuni namba mbili, Second Rule….HAKUNA JAMBO LILILO DHAHIRI MAISHANI. KILA JAMBO NI FUMBO. EVERYTHING IS A SECRET. NOTHING IS AS IT SEEMS.







    Nikazima simu baada ya kutuma ujumbe na kuingia bafuni.





    Mikaka mitatu iliyopita nilipoisambaratisha jumuiya ya siri ya The Board moja ya mwanachAma wa jumuiya hiyo ambaye alitakiwa kwenda gerezani alikuwa ni Zephania Zuberi, kipindi hicho akiwa ni mbunge wa jimbo la Nkasi. Moja kati ya maajabu ya maisha niliyowahi kuyaona ni namna ambavyo Mhe. Zephania Zuberi aliweza kushinda ile kesi dhidi ya jamuhuri na hatimaye chama chake kufanikiwa kushika dola na yeye kuchaguliwa kuwa Waziri Mkuu na yote haya yamefanyika ndani ya miaka mitatu pekee.







    Japokuwa kwa sasa likuwa ameshikilia nafasi hii nyeti ndani ya nchi lakini kutokana na vitu nilivyokuwa navifahamu nay eye alikuwa bado havifahamu na alihitaji kuvijua kutoka kwangu ndicho hasa ambacho kilikuwa kinamfanya ashindwe kunidhuru au kunifanyia lolote baya licha ya kutamani kufanya hivyo.







    Kwa siku mbili zilizopita nilikuwa nimehama kutoka Dodoma Hotel na kuhamia Samali Lodge iliyoko mtaa wa Kiwanja cha ndege hapa Dodoma, sehemu ambayo miaka mitatu iliyopita mimi na Cheupe tulifikia pia tulipokuwa tunawakimbia watu wa jumuiya ya siri ya The Board.







    Asubuhi ya leo nilikuwa nimepokea simu kutoka kwa Kaburu kunieleza kuwa kikao changu nilichokiomba na Waziri Mkuu Zephania Zuberi kilikuwa kimefanikiwa na siku ya leo ndio tunatakiwa kuonana. Mahala ambapo tulikubaliana kuonana ilikuwa ni nyumbani kwake eneo la Mlimwa, muda wa usiku baada ya saa tano kamili.







    Mbele yangu yalikuwa yamebakia masaa mawili tu kufika saa tano kamili usiku, nilikuwa natembea kwenye barabara ya vumbi yenye kuzungukwa na kijimsitu kidogo ambayo ilikuwa inatokea Kiwanja cha ndege. Barabara hii ndio ilikuwa inaenda kukutana na barabara nyingine ndogo ya Lami ambayo ndiyo hasa ilikuwa inaelekea moja kwa moja mpaka Mlimwa hapa Dodoma ambako kuna makazi ya Waziri Mkuu. Kichwani mwangu nilikuwa nafikiria ni kwa sababu gani mpaka muda huu wawakilishi wa Citibank na LE BLOC walikuwa hawajawasiliana nami ilhali walikuwa wanatakiwa wawepo kwenye kikao hiki. Kwa upande fulani kichwani mwangu nilikuwa nahisi kuwa wale mabinti wawili, yule mzungu na mwenzake wa Kinyarwanda walikuwa ndio wawakilishi nilikuwa nawategemea. Lakini kila nilipowaza hili nilijikuta najikosoa mimi mwenyewe kwamba yawezekana si wao kutokana na mwenendo wao wa kunichunguza kwa siri na kutojitambulisha kwangu.







    Karatasi ambazo SIwatu aliziacha pale chumbani kwangu Dodoma Hotel siku mbili zilizopita hazikuweza kunisaidia sana, kwani hazikuonyesha hasa mabinti hao walikuwa ni akina nani, bali zilionyesha mwenendo wa mabinti hao kwa muda wa siku nne ambazo walikuwa pale Hotelini. Yaani walikuwa wanaamka saa ngapi, wanatoka Hotel saa ngapi kwenda kutembea mtaani, wanarejea saa ngapi, wanakula chakula saa ngapi, wanakula nini na kadhalika na kadhalika.



    Japokuwa taarifa hizi hazikunisaidia chochote kwenye kujua hasa wale mabinti walikuwa ni akina nani, lakini ziliniachia swali kichwani Siwatu alizipata wapi zile taarifa? Kama alizikusanya yeye mwenyewe, je alikuwa anazikusanya na kufanya hivyo kwa dhumuni gani hasa? Huyu Siwatu kwa uhalisia wake alikuwa ni nani?







    Sikutaka kujichosha sana akili yangu kwa maswali na vitendawili vingi ambavyo nilikuwa naviwaza kichwani mwangu. Nilidhamiria kuelekeza akili yangu kichwani kuwaza kikao kilichopo mbele yangu. Kikao changu na Waziri Mkuu Zephania Zuberi. Japokuwa mpaka muda huu, masaa mawili kabla ya kikao bado hakukuwa na dalili yoyote ya muwakilishi wa Citibank au LE BLOC, lakini Kaburu alinieleza kwamba, wamemuhakikishia kuwa watakuwepo kwenye kikao na wawakilishi wao tayari wako Dodoma.







    Kichwani nilijiaminisha zaidi kuwa ni wale mabinti wawili. Lakini swali bado lilinaki kichwani, kwanini walikuwa hawajitambulishi kwangu? Na kwa nini walikuwa wananifuatilia kwa siri siri?











    Nikiwa bado natembea kwa mguu tayari nikiwa nimekamata barabara ndogo ya lami ambayo inaenda moja kwa moja mpaka Mlimwa… ghafla gari aina ya Range Rover nyeusi, ilinipita kwa kasi kubwa sana huku vioo vyake vyeusi visivyoonyesha ndani vikiwa vimefungwa. Kwa fikira ya haraka haraka niliamini kuwa gari hii ilikuwa inaelekea nyumbani kwa Waziri Mkuu.



    Pale Mlimwa mahala ambako kuna nyumba ya Waziri MKuu, imejengwa kwenye muinuko fulani hivi kama mlima. Kutoka hapa ambako nimesimama mpaka nyumbani kwa Waziri Mkuu kulikuwa na kama kilomita tatu au mbili na nusu hivi. Kabla ya kufika kwenye makazi hayo, kutoka hapa nilipo kulikuwa na kona moja ya mwisho ambayo nayo inapita kwenye kijimsitu kidogo. Kwa hiyo kama gari likitangulia mbele yako kwa mita kadhaa, labla mita mia mbili au mita mia tatu, kisha likakata kona hii, mara moja linapotea kwenye upeo wa macho yako lakini unakuja kuliona tena kwa mbali sana lianza kukaribia kwenye Makazi ya Waziri Mkuu kutokana na kuwa mlimani.







    Kwa hiyo gari hii aina ya Range Rover iliponipita tu na kukata kona ilipotea kwenye upeo wa macho yangu na kwa kuzingatia kasi ambayo ilikuwa inaendeshwa, nilitegemea ndani ya kama dakika mbili hivi au tatu nianze kuiona kule mlimani ikikaribia kwenye nyumba ya Waziri Mkuu. Lakini zilipita mpaka dakika tano nzima bila kuona gari ile ikitokea kule mbele mlimani. Kwa haraka nikang'amua kwamba gari hii baada ya kukata kona na kuingia kwenye kijimsitu kidogo kilichopo mbele yangu, kuna mahala ilikuwa imesimama. Ni kwasababu gani ilikuwa imesimama, sikuweza kujua kwa haraka, lakini 'machale' yalikuwa yameanza kunicheza.







    Nikatembea kama mwendo wa dakika tano nikaiona gari ile imeegeshwa pembezoni mwa barabara mbele yangu. Bila shaka yoyote nilijua kabisa kuwa yeyote yule ambaye alikuwa anaendesha gari hili alikuwa na malengo fulani na mimi.



    Nilipoifikia gari pale ilipo, licha ya kiza kinene ambacho kilichopo hapa kwenye hiki kijimsitu, nilijitahidi kuchungulia ndani ya gari na kugundua mkuwa kulikuwa hakuna mtu. Aliyekuwa anaendesha hii gari alikuwa ameshuka na sikuweza kumuona kokote pale karibu na gari hii. Taa za mbele za gari zilikuwa zimeachwa zinawaka mwanga mkali kabisa.







    Kitu cha kwanza ambacho nilikifanya ni kupeleka mkono wangu mpaka kiunoni ambako nilikuwa nimeficha silaha yangu, bastola aina ya glock 19 na kisha kuichukua na kuishikilia mkononi. Kisha kwa makusudi kabisa niliendelea kutembea kuelekea mbele huku ule mwanga wa taa za gari ukinimulika. Yeyote yule ambaye alikuwa anafanya mchezo huu nilitaka afahamu fika kwamba nilikuwa na silaha na nilikuwa tayari kuitumia endapo itanibidi kufanya hivyo.







    Niliendelea kutembea kuelekea mbele kufuata barabara hii ya kuelekea kwa Waziri Mkuu kwa takribani dakika nyingine kumi na nikahisi kwambu kulikuwa na mtu au watu ambao walikwa wananifuatilia nyuma yangu kwa kujificha. Hivyo kwa haraka sana nikafanya uamuzi wa kuchepuka na kuingia vichakani. Baada nya kuingia vichakani, nikaanza ukimbia kuelekea mkono wa kulia badala ya kuelekea mbele nilikokuwa naenda. Nilikimbia kuelekea kulia kwa kama dakika tatu nzima na kisha nikaanza kukimbia tena kurudi nyuma nilikotoka bila kutumia barabara, yaani nilikimbia vichaka kwa vichaka. Nilikimbia kwa takribani dakika tano nyingine. Kicha nikatembea mpaka bararabari na kuhama upande wa bara bara, yaani mwanzo nilikuwa upande wa kushoto, na sasa nikahamia vichaka vya upande wa kulia.







    Baada ya hapo nikaanza kutembea kuelekea mbele kuifuata muelekeo wa nyumba ya waziri mkuu. Mpaka hapa nilijua kabisa kuwa yeyote yule ambaye alikuwa ananifuatilia, kwa kitendo hiki cha ghafla nilichokifnya kwa kukimbia kwenye mzunguko wa mvurugiko pamoja na giza hili lazima atakuwa nimempoteza na hakuwa anafahamu niko wapi. Tumaini langu sasa lilikuwa ni kutafuta na nianze kumfuatilia yeye au wao.







    Nilitembea kuelekea mbele kama dakika saba au nane ndipo nikaanza kuona vivuli vya watu wawili mbele yangu kama mita mia moja kutoka nilipo nao wakiwa vichakani wanatafuta kitu. Walikuwa wananitafuta mimi.







    Niliwafuatilia kwa kama dakika tano nyingine, nikagundua kuwa walikuwa wanazunguka hapo hapo tu, hawaelekei mbele nilikokuwa nataka. Kwa hesabu ya haraka nilijua kuwa nimebakiwa na kama chini ya saa moja mbele yangu kufikia mihadi yangu na kikao changu na Waziri Mkuu, kama nitaendeleza huu upuuzi unaoendelea hapa tunaweza kujikuta tunawindana mpaka asubuhi kunakucha.







    Japokuwa wote tulikuwa gizani, lakini kwa madakika yote haya ambayo tumekaa hapa gizani, nilijikuta macho tayari yamezoea giza na nilianza akuona kwa usawia. Kwahiyo nikainua bastola yangu kwa kujiamini kabisa na kumlenga mmoja wa wale watu akiwa kama mita thelathini mbele yangu, nililenga pajani kwa ke kwa makusudi kabisa ili nimjeruhi tu bila kumsababishia jeraha linaloweza kusababisha kifo.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/





    "Baaaaaaaaannnggg.!!"







    Nilifyatua risasi na ilimpata barabara nilipokua ninapataka. Nilitegemea nao watajibu mapigo ya risasi, hivyo baada ya kufyatua risasi hii nilijificha nyuma ya mtu. Dakika nzima ilipita bila kusikia majibu yoyote yale ya riasi kutoka kwao. Nilichokuwa nasikia ni kelele za malalamiko ya maumivu tu kutoka kwa yule ambaye nilimdungua na mwenzake alikuwa anaonekana kama alikuwa anamsaidia kumnyanyua au kumburuza kutoka pale walipo.







    Kwa kuwasikiliza tu sauti zao, niligundua kuwa waliuwa ni wanawake na wote wawili walikuwa wanazungumza kifaransa. Niljikuta ghafla nimeshikwa na bumbuwazi baada ya akili yangu mara moja kung'amua kuwa hawa watakuwa ni wale mabinti wawili ambao walikuwa wananifuatilia kwa wiki nzima iliyopita pale Dodoma Hotel. "hawa mabinti wanataka nini?" nilijikuta najiuliza tena na tena kichwani.







    Nilianza kusikia sauti zao sasa zinasikika kutoka barabarani, na nikahisi kuwa walikuwa wanataka kupakiana kwenye gari lao na kuondoka hapo kabla sijafanya madhara makubwa zaidi. Bila kupoteza muda mara moja nikatimua mbio kuelekea barabarani walipo.







    "simameni hapo hapo mlipo kabla sijawapasua vichwa.!!" Nilikuwa naongea kwa kufoka huku nawafuata pale walipo.







    "put the gun down you idiot.!" Moja ya wale akina dada aliongea kwa kingereza chenye lafudhi ya kifaransa.







    "I say no body moves!" nikafoka zaidi huku nimewakaribia kabisa.







    "Ray nimekwambia weka silaha yako chini!" yule binti mmoja ambaye alikuwa ni yule wa Kinyarwanda aliongea kwa kishwahili fasaha huku amenikazia macho.







    Macho yetu yalikuwa yamezoea giza tayari, kwahiyo tulikuwa tunaonana kwa usahihi kabisa. Tulikuwa umbali wa kama mita mbili tu hivi, alipotamka jina langu na kunikazia macho alionekana dhahiri kabisa alikuwa ananifahamu na hawakuwa na nia mbaya dhidi yangu japokuwa nilijua pasina shaka kabisa kulikuwa na jambo fulani hivi la siri ambalo litawawia vigumu sana kuniambia ukweli.







    "whoa re you guys? And what the hell do you want? You guys have been following me for the whole week.!! What the hell do you want?" nikang'aka kwa umombo.







    "you know exactly who we are… so stop playing around!"







    "who is playing around!! I don't know who you are… so I'm going ask you one last time… who are you?"







    Ukapita ukimya wa kama dakika mbili nzima tukiwa tumekaziana macho. Bado nilikuwa nimewanyooshea bastola huku kidole kikiwa kwenye 'trigger'. Yule mwenzake pale chini alikuwa anagugumia bad na maumivu ya jeraha la risasi.







    "Representatives from LE BLOC and Citibank!" yule binti akaongea kwa hasira kwa kifupi tu akiwa bado amenikazia macho.







    "and why didn't you just approach me and say so, all these days ?" nikauliza huku nimeanza kushusha chini bastola yangu.







    "we have our reasons!" yule binti wa Kinyarwanda alinijibu bila kuniangalia huku anamuinua mwenzake na kumuweka kwenye siti ya nyuma ya gari.







    "like what?" nikamuuliza huku narudisha tena bastola yangu kiunoni.







    "..Lets see… unh for 'starters', we don't trust you and may be I could say we don't know you..!" aliongea huku anaanza kufungua mlango wa mbele wa gari wa siti ya dereva.







    "…what the hell are talking about! How can you say that you don't know me while you said my name a few seconds ago?"







    "its complicated! Lets get the hell out of here before someone find us!"







    Akawasha gari na kukata kona kushoto kutoka barabarani kuelekea vichakani. Aliendsha kwa mwendo wa taratibu wa tahadhari kutokana na miti miti mingi hivyo niliweza kulifuatia gari kwa nyuma kwa miguu. Tuliingia ndani ya vichaka kama mwendo wa dakika tatu kutoka barabarani na kisha akasimamisha gari na kisha kufungua mlango wa nyuma aliko mwenzake ili apate hewa safi ya kutosha.



    Nikapiga tena hesabu haraka haraka kichwani, itakuwa imebakia kama nusu saa tu ili kufika saa tano kamili ambapo tunapaswa kuonana na Waziri Mkuu.







    Yule binti wa Kinyarwanda akachukua begi la mgongoni kutoka katika siti ya nyuma ya gari na kuanza kutoa vifaa vya kurekodia. Nilielewa ni nini alikuwa nataka tufanye. Alikuwa anataka rekodi ya uthibitisho kuhusu uhalali wangu… aikuwa anataka recording namba 004W22 katika mfululizo wa recording nilianza kuziwasilisha LE BLOC na Citibank tangu mwaka na nusu uliopita. Mwezi mmoja uliopita niliwasilisha recording namba 004W21 na sasa ilikuwa ni recording ya tatu kutoka mwisho, 004W22. Kilichoukuwa kinanikera rohoni kwangu ni kwamba kazi hii ya kurekodi tulitakiwa kufanya siku kadhaa zilizopita, lakini ajabu walikuwa wananipiga chenga mabinti hawa. Nilijisikia kukereka haswa kila nikizingatia kwamba pia tulikuwa na dakika chache sana mbele yetu tunatakiwa kuwa mbele ya kikao.











    "ok! We are all set.. lets do this quickly" binti wa Kinyarwanda aliongea huku amewasha camera iliyo juu ya stendi yake na kunimulika na taa ya kurekodia.







    Sikutaka kupoteza muda… moja kwa moja nikaenda kwenye zoezi lililo mbele yetu.







    "Jina langu naitwa Rweyemamu Kajuna, hii ni recording namba 004W22 kuthibitihs nina password ya sanduku 7712/LH"







    Yule binti alikuwa amenikazia macho ya kukereka nilipomaliza kujieleza sentesi hii.







    "Nini?" Nikamuuliza.







    "not good enough!" aliongea kwa lafudhi yake ya kifaransa.







    Rohoni nilikereka zaidi. Kwanza nilikereka kwa kunitaka nifanye zoezi hili leo lakini nilikereka pia nikijua wazi kabisa binti huyu hakuwa hata akijua ni nini hasa nilikuwa naongea. Niliamini kabisa alikuwa hata hajua hiyo 'recording namba 004W22' ilikuwa na maana gani. Niliamini tu kuwa alikuwa amekaririshwa natakiwa nijieleze vipi kwenye recording hii. Nilikereka zaidi kila nilipokumbuka kwamba tulikuwa tunachelewa kwenye kikao na Waziri Mkuu, na si hivyo tu nilihofia juu ya uhai wa mwenzake ambaye alikuwa pale kwenye gari anaugulia maumivu.







    "..hivi tutarudia hii kwa mara ngapi ili uridhike.!" Nikajitahidi kumuuliza kwa kujifanya kukereka haswa, lakini ukweli ni kwamba akili yangu na macho yangu vyote vilikua kwenye mlango wa gari ulio wazi kama mita tano kutoka pale tulikosimama.







    "…tutarudia mara nyingi kadiri ambavyo utaendelea kunizungusha.!" Yule dada naye akaongea kwa ukali kiasi na safari hii kunifanya nihisi hisia ya kukereka kwenye sauti yake.







    Sikumjibu chochote moja kwa moja, akili yangu na macho yangu bado vilikuwa kwenye ule mlango wa gari mbele yetu. Nikaanza kuhisi labda huyu binti hajui mwenzake yuko katika hali tete kiasi gani. Lakini kwa kadiri nilivyomsoma juu ya weledi wake wa matumizi ya silaha ilinifanya niondoe hisia za kudhania kuwa labda binti huyu alikuwa hajui hali tete aliyonayo mwenzake pale kwenye gari. Silaha ambayo nilitumia kufyatua risasi aliiona na ilikuwa pale ndani ya gari, bastola aina ya glock 19 na nilikuwa na uhakika kabisa alikuwa anajua madhara ambayo bastola hii inafanya kwenye mwili wa binadamu ikifyatuliwa umbali wa karibu kaka ambavyo mimi niliifyatua.







    "…mwenzako kama hatutampatia huduma ya kwanza ndani ya dakika chache zijazo tutampoteza.!" Nikaongea tena kwa mara nyingine huku bado macho yangu nimekaza kuelekea kule ambapo mlango wa gari ulikuwa umefunguliwa.







    Hakunijibu chochote kile. Aliendelea tu kunikazia macho. Endapo kama tutaendelea na huu mchezo, ni dhahiri kwamba tutakosa kikao na Waziri Mkuu na pia mtunaweza kumpoteza yule binti wa kizungu ambaye niliamini alikuwa na taarifa nyeti ninazohitaji. Nikakata shauri nijieleze kwa ufasaha kwa kadiri anavyotaka.







    "Jina langu naitwa Rweyemamu Charles Kajuna, watu wa karibu wanapendelea kuniita Ray na marafiki zangu wanapendelea kuniita jina la utani 'Kichwa'… hii ni recording namba 004W22 kuthibitisha kuwa ninayo mkononi mwangu password ya sanduku 7712/LH lililopo Union Bank Of India, jijini Mumbay nchini India. Narudia hii isomeke kama recording namba 004W22.!"







    Nikamaliza na kumuangalia usoni yule binti huku nimeamkazia macho, "Umeridhika?" nikamuuliza nikiwa nimekereka haswa.







    "Angalau inaridhisha kwa utambulisho.!" Akanijibu huku kwa mara ya kwanza nikimuona akitabasamu.











    ********







    SASA HIVI (KWENYE MAKAZI YA WAZIRI MKUU - MLIMWA, DODOMA)











    Wote wanne, mimi, Giselle, Ilana na PM Zephania tulikuwa tumekaa kwenye mukimya wa kama dakika mbili nzima pale sebeleni.







    PM Zephania alikuwa anitazama huku usoni kama vile ana tabasamu la mbali sana kuashiria kama vile amepata ushindi fulani hivi.







    "Ray, nahisi nafahamu ni kwanini uko hapa, na nahisi nafahamu hiki kikao kina lengo gani haswa… lakini kwa faida yetu sote nadhani unieleze kinagaubaga kabisa kila kitu kuhusu lengo la hiki kikao na ni nini hasa kimekusukuma mpka mkufikia hapa leo kwenye kikao hiki.!"







    PM zephania aliongea kwa kujiamini na kisha kuinua kikombe cha kahawa alicholetewa muda si mrefu na kunywa kidogo.











    Nilielewa ni nini hasa napaswa kueleza… japokuwa nilijua mengi tayari atakuwa anayafahamu lakini nilitakiwa nimueleze kila kitu kuanzia safari yangu ya Zurich miaka mitatu iliyopita, nimueleze kuhusu nilichokikuta kwenye sanduku la siri la mwenyekiti wao lilikuwa linahifadhi nyaraka huko Zurich kwenye tawi la bank ya Citibak, nimueleze pia matukio yote yaliyotokea kwa miaka miwili iliyopita na kunifanya nichukue maamuzi haya ambayo niko nayatekeleza na ambayo yanaweza kabisa kupelekea kuunda upya jumuiya ya siri ya 'The Board'… na mwisho kabisa nimueleze kwa nini nimekuja kuonana naye.







    Kwa haraka haraka, naweza kuonekana mwendawazimu kwa kutaka kuunda tena upya jumuiya ambayo nilipambana kufa na kupona kuisambaratisha miaka mitatu iliyopita. Na kwa adui yangu kama PM Zephania anaweza kuhisi labda amenishinda kwa kitendo changu cha kuja kuonana naye.



    Lakini kitu ambacho hakijui ni miaka mitatu iliyopita, baada ya safari yangui ya Zurich, nilijiwekea kanuni tatu kuongoza maisha yangu. Three Rules. Na kanuni ya tatu, nilijiapiza kuwa… NITAISHI KILA SIKU YANGU KIMKAKATI… AS A BORN TACTICIAN… KILA HATUA NITAKAYOPIGA INA MAANA TOFAUTI NYUMA YA PAZIA. .. "EVERY MOVE MEANS SOMETHING."





    Waziri mkuu Zephania Zuberi alikuwa ananitazama huku anatabasamu baada ya kuniomba nieleze kwa undani kuhusu dhamira yangu ya kufika hapa nyumbani kwake leo hii na nini hasa kilikuwa kimetokea mpaka kupata msukumo huu wa kunifanya nimfuate licha ya uadui wetu ulio wazi kabisa.







    Nilielewa kuwa swali hili lilikuwa na mtego ndani yake na lingenifanya kueleza mambo ambayo katika namna ya kawaida nisingeliweza kuyaeleza. Lakini nilijua fika kwamba kama sitaeleza masuala haya kuna uwezekano mkubwa kwangu kushindwa kutimiza dhamira ambayo imenileta hapa.







    “Sawa muheshimiwa… nitaeleza kila kitu ambacho kimetokea miaka miwili au mitatu iliyopita na kufanya tuwe hapa kwako elo hii.!”







    Nikavuta pumzi ndefu ndani na kuishusha… nikakaa sawia pale kwenye kiti.







    “Lets start from the beginning.!”















    MIAKA MITATU ILIYOPITA







    Nilikuwa nimewasili kwenye chumba changu cha Hotel hapa jijini Zurich kama dakika arobaini zilizopita kutokea uwanja wa ndege wa Zurich hapa nchini Uswisi. Safari hii ya masaa karibia nane na dakika hamsini kutoka Dar es Salaam mpaka hapa ilikuwa imenichosha haswa na nilikuwa nahitaji kupumzika vya kutosha kabla ya kuanza ratiba nyingine yeyote ile. Nilikuwa nimetumia dakika arobaini zote tangu nimefika nikiwa ndani ya bafu sio tu nikioga bali pia nikitafakari hatua kwa hatua vitu ninavyo takiwa kuvifanya nikiwa hapa. Kila kitu ambacho nilitakiwa kukifanya nilipaswa kukifanya kwa ukamilifu wa hali ya juu pasipo chembe ya hitilafu au kukosea.







    Saa yangu mkononi ilikuwa inaniambia ilikuwa yapata saa kumi na moja jioni na nilikuwa katika dirisha langu la chumba cha hoteli maarufu niliyofikia hapa Zurichinayoitwa Radisson Blu Hotel ambayo iko mtaa wa Fracht Magharibi (freacht west) takribani kama kilomita kumi kutoka uwanja wa ndege wa Zurich. Japokuwa macho yangu pale dirishani yalikuwa yanafurahia kutazama uzuri wa muonekano wa jiji hili lenye kupendeza hasa, lakini akili yangu na fikira zangu zilikuwa mbali mno nikitafakari leo usiku nitakapo kutana na mtu ambaye nilimfahamu kwa jina moja tu la Hudini. Sikujua kama mtu huyu ni mwanamke au mwanaume, kijana au mzee. Nilichokuwa nakijua tu ni kwamba yeye ndiye mtu wa kwanza kabisa ambaye napaswa kuonana naye baada ya kufika hapa Zurich.







    Nikatoka dirishani na kusogea tena mpaka kwenye meza iliyomo humu chumbani ambayo juu yake nilikuwa nimeweka bahasha ambayo miezi kadhaa iliyopita nilikabidhiwa na baba yangu Dodoma dakika chache kabla hajajiua kwa risasi mbele ya macho yangu. Ni bahasha hii ambayo siku ile aliponikabidhi alinieleza kuwa anataka nifuate maelezo ambayo yalikuwa ndani yake na nije hapa Zurich kwa ajili ya lengo ambalo alikuwa amelipanga.







    Siku ile Dodoma sikudhani kama itakuja kutokea maishani mwangu siku moja nikafika hapa Zurich kutokana na kutimiza matakwa ya baba yangu kunitaka nifike hapa. Lakini binadamu wote tumeumbwa na laana kubwa kuliko zote, laana ambayyo muda mwingi huwa tunaihesabu kama Baraka au ubora wa binadamu… shauku… curiosity! Japokuwa shauku ndiyo imetufanya binadamu kuimiliki dunia na kuielewa kuliko viumbe vingine vyote, lakini pia shauku ni moja kati ya laana kubwa zaidi ambazo ziko ndani ya ubongo wetu. Unapopata wazo fulani, au kutaka kujua kitu fulani, shauku inayotengenezeka kwenye nafsi inakuwa kama vile muwasho wa upele ambao hautapoa mpaka ukiukuna.







    Shauku ndiyo iliyonifanya licha ya kupita miezi takribani minne bila kuifungua bahasha hii niliyopewa na baba yangu, hatimaye nikaifungua na kusoma kilichomo ndani. Siku ambayo nilifungua bahasha ile, ndiyo siku ambayo nami laana hii ya shauku ilipanda mbegu ndani yangu ya kutaka kujua undani hasa wa suala nililoliona na kunifanya leo hii kuwa hapa Zurich.





    Nakumbuka kwa ufasaha kabisa siku ile ya kufungua bahasha jinsi ilivyo kuwa. Ilikuwa imepita miezi mine tangu siku ile Dodoma porini kwenye kijumba cha mbao ambapo mzee wangu alinikabidhi bahasha. Siku hii niliyofungua bahasha ilikuwa muda wa usiku wa manane kama saa saba hivi. Siku hii nakumbuka kabla ya kulala nilikuwa nimezozana mno na Cheupe, Hasnat, mama mtarajiwa. . Mzozo wenyewe ulianza kama suala la kawaida tu… Cheupe alikuwa amenieleza kuhus ‘offer’ ya kazi ambayo alikuwa ameipta Nairobi na alikuwa anatakiwa kwenda kuripoti miezi mitatu kutoka sasa, siku hiyo ambayo alikuwa ananieleza. Nilimkatalia kata kata kwa kuzingatia uhalisia kwamba ulikuwa umebakia mwezi mmoja kabla ya kujifungua. Hii ilimaanisha kwamba ingempa miezi miwili tu ya kupimzika na kisha asafiri kwenda Nairobi kwa ajili ya kazi. Nakumbuka nilifoka haswa kuwa kama anataka kazi basi asubiri walau mtoto afikishe mwaka mmoja ndipo hapo aanze hizo harakati zake za kufanya kazi. Naye alifoka kweli kweli kwamba licha ya kumuhudumia kila kitu lakini kama msichana msomi hawezi kukaa bure nyumbani akisubiri kuzeeka, anataka atumie ‘potential’ aliyo nayo. Japokuwa nilimuelewa hoja yake hii ya kutaka kujishughulisha lakini bado nilishikilia msimamo wangu kuwa hawezi kuanza kazi mpaka mtoto atakapofikisha mwaka mmoja.



    http://pseudepigraphas.blogspot.com/



    Mabishano yalipo pamba moto haswa nakumbuka Cheupe alitamka neno ambalo liliuchoma moyo wangu kuliko ambavyo alifikiria, aliniambia kukwa “Ray siku zote huwa hauelewi hisia za wengine… its always about you!” Mneno haya yalinichoma sio moyoni tu bali nilisikia maumivu yake mpaka kwenye mifupa ya mwili. Nilijikuta mwili wote umeniishia nguvu nikitafakari kauli hii… ati mimi sizingatii hisia za wengine? Ati mimi siku zote najali kuridhisha nafsi yangu tu? Mimi huyu? Mimi Ray au mtu mwingine?





    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog