Search This Blog

Sunday 20 November 2022

NYUMA YAKO (3) - 5

 







    Simulizi : Nyuma Yako (3)

    Sehemu Ya Tano (5)







    **



    Saa nne asubuhi …





    Bwana James alinyoosha miguu yake akiwa anapitia riwaya ya Sherlock Holmes. Macho yake yalikuwa yapo bize kana kwamba anatazama habari fulani makini. Aligeuza kurasa na kurasa.



    Alijikuta anasahau hata kama kuna kikombe chake cha kahawa mezani. Kahawa ilikuwa inaelekea kupoa.



    Kuzubaa kwake huko kulikuja kuharibiwa na hodi mlangoni, akabandua macho kitabuni kuangaza. Kidogo bwana Smith akaingia akiwa ameshikilia kitambaa cha kujifutia jasho. Bwana huyo alikuwa anatota isijulikane kwanini.



    Macho yake yalikuwa yameingia ndani, uso kukurukakara.



    Aliketi kwenye kiti kisha akajifuta jasho akimsalimu James.



    “Vipi?” James akauliza akiweka riwaya yake kando. “Kuna tatizo?”



    “Nadhani lipo,” akasema Smith. “Kuna mambo kadhaa yametokea nimekuja kuyapatia majibu.”



    Bwana Smith aliposema hayo akatoa simu yake, akaifungua na kumkabidhi James. James alipoangaza akaona sura ya Marshall.



    “Unamjua huyo sio?”



    “Ndio, yu kwenye kesi yangu.”



    “Swadakta. Bwana Ian amemtaja mtu huyo kuwa ndiye aliyevamia makazi yake na kufanya mauaji.”



    “Najua.”



    “Unajua? Mbona hukunambia hapo kabla?”



    James akaweka simu kando. Akamtazama bwana Smith huku akifumba mikono yake. “Smith, nadhani cha muhimu hapa ni kujua kwanini Ian amevamiwa. Kwanini bwana Marshall, mtuhumiwa wa kumpoteza Raisi, akamshambulia kumteka na mwisho wa siku kumteka.



    Vipi umepata lolote kuhusu hilo?”



    “Kiasi,” Smith akajibu akivuta simu yake. “Tumefanya mahojiano kidogo lakini hakufunguka sana kwa kudai mpaka mwanasheria wake atakapowasili.”

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    “Mwanasheria?”



    “Ndio.”



    “Hajaongelea lolote kuhusu kutekwa kwake na kutupwa?”



    “Ndo’ amesema waliomteka ni Marshall na wenzake. Hakuna cha ziada.”



    Smith akafuta jasho kwenye paji lake la uso. Akamtazama James aliyekuwa kwenye mafikirio alafu akamuuliza, “Vipi? Una jambo?”



    “Hao watu waliomteka watakuwa na taarifa zaidi kumhusu Ian,” James akasema akitazama dirisha la ofisi. Uso wake ulikuwa mtulivu.



    “Ni sahihi. Lakini sasa tutawapatia wapi? Ndo’ maana nikakuletea hiyo picha unipe maneno.”



    James akafikiri kidogo kisha akashusha pumzi.



    “Nadhani kuna mahali tunaweza kupata taarifa zaidi.” aliposema hivyo akanyanyuka na kubandua koti lake kwenye kiti kujiveka, “Tuongozane.”





    **



    Saa tano na nusu …





    “Madam, kuna intake zingine tatu zimeingia,” alisema sekretari akimkabidhi miss Danielle bahasha.



    “Nashukuru, waweza kwenda.”



    Miss Danielle akapokea bahasha hizo na kuziweka mezani.



    “Wamesema zinahitajika upesi.”



    “Sawa. Waweza tu enda hamna shida.”



    Sekretari akaenda zake akimwacha Danielle akitazama tarakilishi yake. Mwanamke huyo alikuwa amevalia suti rangi ya cream iliyomkaa vema mwili. Nywele zake hakuzibana, bali ameziacha zikimwagikia mgongoni. Na macho yake ameyafunika kwa miwani ya kumsaidia kulinda macho dhidi ya mwanga wa tarakilishi.



    Kidogo, akaacha kutazama tarakilishi na kupekua bahasha ile aliyoletewa. Zilikuwa ni bahasha za maombi ya upelelezi kwenye mambo kadha wa kadha.



    Basi baada ya kuzisoma, akanyanyua simu yake na kumpigia jamaa mmoja aitwaye Timoth. Jamaa huyo ni moja ya wataaluma wa sayansi ya kipelezi. Mmoja ya watu anaofanya nao kazi.



    “Timoth, nakuhitaji mara moja ofisini,” alisema Danielle. “yah … kuna kazi kadhaa hapa zimekuja pamoja na muanisho wa malipo yake na malipo ya awali. …”



    Akiwa anaendelea kuongea, macho yake yakatazama kwenye runinga inayopokea taarifa toka kwenye kamera za cctv ambazo zimepachikwa eneo lake la kazi.



    Alipotazama vema, akamwona bwana James akiwa ameongozana na mtu mwingine ambaye hakumtambua. Basi akamaliza maongezi yake na kuketi kumngoja mgeni.



    Lakini akiwa na maswali kidogo kichwani. Alijiuliza kama bwana James atakuwa amekuja hapo kwa ajili ya kesi ya ile nyumba iliyolipuliwa na Kelly.



    Kidogo sekretari akaingia na Danielle akampatia ishara ya kichwa kumruhusu mgeni apite.



    Bwana James akiwa ameongozana na Smith wakasalimiana na Miss Danielle kisha wakaketi.



    “Niwie radhi miss, ujio wangu umekuwa wa ghafla pasipo kutoa taarifa. Naamini sijakukwaza sana,” alisema bwana James.



    “Usijali, karibuni.”



    “Nashukuru. Huyu ni mwenzangu, anaitwa inspekta Smith. Tusingependa kukupotezea sana muda wako maana bila shaka umetingwa. Tupo hapa kwa ajili ya kesi ya bwana Ian Livermore.”



    Miss Danielle akavua miwani yake na kuiweka mezani. Akamtazama bwana James kwa umakini.



    “Nadhani wewe si mgeni wa hizi habari. Tumemtia Ian mikononi lakini bado kumekuwa na shida sana kwenye swala la kupata taarifa toka kwake. Tunaamini atakuwa na taarifa nzito. Vipi hakuna namna ambavyo unaweza kutusaidia?”



    Danielle akakunja sura yake kidogo, “sijawaelewa maafisa. Kuwasaidia kuhusu nini yani?”



    “Wakati tulipomtia Ian mikononi ilibainika alikuwa amenyweshwa kiasi kikubwa cha Sodium thiopental. Bila shaka huko alipokuwa alibwabwaja mengi kwa kupumbazwa na kilevi hicho…”



    “Kwanini nanyi msikitumie afisa?” Danielle akauliza akinyakua bahasha yake na kuifunga vema.



    “Unajua ni kinyume na sheria kutumia mbinu hiyo ndani ya Marekani,” alisema James kisha akanyamaza. Ukimya wake ukamfanya Danielle amtazame.



    “Naamini utakuwa unajua kitu,” akasema James. “Tunaomba utusaidie.”





    **



    *SEHEMU YA 27*



    Japo walimbembeleza Danielle, mwanamke huyo hakuridhia kwamba ana kitu, alikataa katakata na basi wapelelezi hao wakaondoka na kwenda kujitweka kwenye gari lao.



    “Hamna kitu, James. Tumepoteza tu muda bure.”



    “Hapana,” James akasema akitikisa kichwa. “Unadhani yeye ni mjinga? Hawezi akatuambia katika namna hiyo.”



    “Kama ulikuwa unajua kwanini tukaja huku?”



    “Tumewekeza, Smith. Tumewekeza hapo na si vinginevyo. Mambo yatakuja, amini nakwambia.”



    Basi wakaondoka zao. Kule ofisini naye Danielle akawa ameachwa katika namna ya maswali. Aliwazia kuhusu ombi la wale watu na basi kidogo akajikuta akimpigia simu Marshall kumweleza kuhusu haja hiyo.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Simu ya Marshall iliita kwa muda kidogo kabla ya kupokelewa. Mwanaume huyo alikuwa ndani ya gari lakini simu ilikuwa ‘silent’.



    “Umemwambiaje?” Marshall akauliza. Kidogo mazingatio yake hayakuwa makubwa. Macho yake yalikuwa bize kutazama jengo fulani. Jengo ambalo Kelly ndipo anaishi.



    “Unadhani itakuwa na maana?” akauliza Marshall. “ … sawa, basi utanambia kitakachotokea,” akahitimisha Marshall kisha akakata simu na kuiweka kwenye kiti cha pembeni.



    Alikaa hapo kwa kama dakika kumi baada ya kukata simu. Alifikiri jambo. Akanyanyua tena simu yake na kumpigia Danielle. Punde simu ikapokelewa.



    “Nazama ndani,” akasema Marshall kisha ashashuka toka kwenye gari akiwa amejiandaa. Nyuma ya kiuno kulikuwa na bunduki ambayo ina risasi tano kwa ajili ya dharura.



    Basi akajongea na kuzama ndani ya jengo. Halikuwa jengo la mtu mmoja, lah! Limepangishwa kwa watu kadhaa akiwemo pia Kelly.



    Marshall akakwea ngazi mpaka kufika mahali alipokuwa anaenda. Mbele kabisa ya mlango wa chumba cha Kelly, hapo akabisha hodi mara mbili kisha akatulia.



    Alilivalia tabasamu na akajitahidi kufanya uso wake usionyeshe shaka.



    “Ni nani?” sauti ikauliza ndani ya kifua cha Kelly. Mwanamke huyo alikuwa yu chumbani akiwa anapakia nguo zake kadhaa kwenye begi dogo.



    Aliacha kila kitu akakodoa macho. Basi kwa tahadhari, akasomba bunduki yake na kuiminyia kwenye mkono wake wa kuume kisha akasonga kuuendea mlango.



    Kabla hajaufungua, akachungulia kwenye kitundu, akastaajabu kumwona Marshall papo. Akajiuliza maswali kadhaa lakini asikae muda akaufungua mlango na kuigiza tabasamu.



    Kila mmoja alikuwa anatabasamu. Matabasamu ya wongo.



    “Marshall!” Kelly alistaajabu. “Umepajuaje hapa?”



    Marshall aliingia ndani mlango ukafungwa. Kelly aliweka nyuma mkono wake uliobebelea bunduki. Mara kadhaa na ule ambao hauna bunduki nao akauweka nyuma ili kuigizia hakuna kitu cha ajabu.



    Alipoketi, akaikalia bunduki hiyo.



    “Nitaachaje kupajua hapa na ingali Jack alikuja?”



    “Oh! Amekuambia?”



    “Hawezi kutoniambia. Nadhani unamfahamu vema.”



    “Ni kweli. Umekuwa ugeni wa kushtukiza kabisa.”



    “Vipi? Ulikuwa na mahali unakwenda kwani?”



    “Aaahmm … hapana. Sema tu sikukutaraji. Si unajua. It is more than a surprise.”



    “Nilihisi utahitaji kuniona ama sivyo?”



    Kelly akacheka kiuongo. Aliporudisha macho yake akamkuta Marshall akiwa anamtazama kwa macho ya mkazo. Kidogo akahofia.



    “Yah! Sijakuona muda, Marshall. Tangu mahakamani.”



    “Ni kweli. Naomba basi unipatie maji ya kunywa. Nimengoja uniulize lakini nimeona kimya.”



    Kelly akatabasamu.



    Alikuwa amekalia bunduki.



    Ni kivipi angesimama?







    Basi akawaza na kuwazua ndani ya muda wake mchache na punde akavuta mto uliokuwepo karibu na kuzuga kuushikashika.



    “Ungependelea maji gani Marshall, baridi ama moto?”



    “Naomba ya baridi.”



    “Yasiwe na ladha yoyote?”



    “Hapana. Maji kama maji tu.”



    Basi Kelly akanyanyuka upesi na kusogeza mto wake pale alipokuwa ameketi. Kisha akaendaze kufuata jokofu na kuthoa maji humo kuyamimina ndani ya glasi na kwenda nayo sebuleni kumpa Marshall.



    “Niambie Marshall. Maisha yamekwendaje? Ni muda mrefu sasa na umepitia mengi hapa karibuni.”



    **



    “Una uhakika?” sauti iliuliza ndani ya simu.



    “Ndio, nina uhakika. Kwa macho yangu nimemwona,” akasema mwanaume mnene aliyevalia shati limembana. Mwanaume huyo alikuwa ana pipi ya kijiti mdomoni, kofia kaigeuzia nyuma.



    Tumbo lake lilikuwa kubwa kiasi kwamba shati halikuwa linamtosha. Jeans yake ilikuwa imepauka na viatu vyake havikuwa inaridhisha.



    “... ameingia ndani ya jengo muda si mrefu. Kwa macho yangu kabisa nimemtambua. Ndiye yeye!”



    “Sawa tunakuja!” sauti ikasema kimamlaka. Bwana huyo kabla hajakata simu, akauliza, “na vipi kuhusu pesa yangu?”



    “Utapata pesa punde tutakampotia mkononi kwa kutumia taarifa yako.”



    Baada ya hapo simu ikakata akibakia mwenye hamu. Alitoa pipi yake mdomoni akajaribu kupiga tena lakini hakupokelewa. Akalaani akiwa amekunja ndita.



    Kwasababu za madai, akakaa kando kungoja wana usalama watakaokuja ili basi apate kuonana nao na kuwadai pesa yake.



    **



    Kelly alicheka akiwa ameziba kinywa chake. Alitengenezea nywele zake vema kisha akamtazama Marshall. “Nadhani utakuwa unatania.”



    “Hapana,” Marshall akatikisa kichwa. “Nipo serious kabisa.”



    Basi Kelly akalifinya tabasamu lake la uongo na kusema, “sijui unachokiongelea, Marshall. Kabisa.”



    “Kwenu ni wapi Kelly?” Marshall akauliza. “Usiniambie New Zealand maana ni wongo.”



    Kelly akamtazama kwanza Marshall. Kuna kitu alikuwa anakiwaza kichwani mwake.



    “Kwanini waniuliza vivyo, Marshall? Unadhani nilikudanganya?”



    “Sidhani bali ni kweli ulinidanganya.”



    “Kwanini?”



    “Sijajua kwasababu gani, Kelly. Labda uniambie lengo lako ni nini haswa? Kuna mtu alikutuma kunifuatilia tangu kule Hong Kong?”



    Kelly akaduwaa. Akatabasamu kiuongo kabla hajatikisa kichwa chake na kutengenezea nywele zake kichwani.



    “Nani amekutuma Kelly. Niambie kweli na sitafanya jambo. Nitakuachia huru uende zako.”



    “Marshall, nimeshasema hapo awali. Sijui unachokiongea. Nilikutana na wewe Hongkong wote tukiwa kwenye utalii. Tumekutana tena Marekani sababu nimekuja kusoma. Hivyo vitu viwili ndo’ vimekufanya uunganishe matukio kiasi hicho?”



    Marshall akazamisha mkono wake kwenye mfuko wa koti alafu akatoa picha aliyoirushia mezani. Kelly akadaka picha hiyo na kuitazama. Ilikuwa ya Keen!



    Hapo mapigo yake ya moyo yakachumpa kabla ya kukimbia. Alihisi mambo mengi sasa. Kwa kufupisha, alijiona hayupo salama tena.



    Akatoa macho yake kwenye picha na kumtazama Marshall, wakakutana macho kwa macho. Kuna kitu kilikuwa kinanenwa japo vinywa vilikuwa kimya.



    Kelly akarejesha macho yake kwenye picha lakini sasa mawazo yake yakiwa mbali. Alikuwa anawaza namna ya kujikomboa ama kummaliza Marshall.



    Kulikuwa kuna kaukimya ka ufu kwa muda kidogo.



    Punde ukimya huo ukavunjwa na mlio wa king’ora cha polisi huko nje. Kila mtu alishtuka. Walitazamana na upesi kila mmoja akatoa silaha yake kumwonyeshea mwenzake. Tendo hilo lilichukua kama sekunde moja tu!



    “Weka silaha chini!” Marshall akafoka, Kelly akabinua mdomo wake na kutikisa kichwa, “weka wewe silaha chini , Marshall,” akasema kwa sauti ya pole.



    Wakiendelea kujibizana, wakasikia sauti za watu zikiwa zinajongea karibu, na zaidi zikiwa zinakwea ngazi.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Walitazamana kwa tahadhari na kidogo tu wakahisi watu wapo mlangoni.



    Mwanaume mmoja aliyevalia sare za kikosi cha kupambana na majanga na maswahiba ya wepesi, alitazama wenzake wanne na kuwapatia ishara. Walikuwa wamebebelea bunduki na vifua vyao vimekingwa na ‘bulletproof’. mmoja kati yao alikuwa amebebelea gogo la chuma kwa ajili ya kuvunjia mlango.



    Wakahesabu moja, mbili, tatu wakavunja mlango na kuzama ndani wakiwa wamenyooshea midomo yao ya bunduki sebuleni. Hawakuona kitu. Wakatoa macho kuangaza na punde yule mmoja wao, captain, akawaagiza wenzake watawanyike kusaka maeneo mbalimbali humo ndani.



    Walisaka kwa kama dakika tatu, hawakupata kitu!



    “Hamna kitu, cap!” alisema bwana mmoja. Captain akatazama dirisha na kugundua lilikuwa wazi. Akasonga na kulitazama, hapo kwenye kingo za dirisha akaona kukiwa kumebonyea.



    Alipotazama kwenda juu, akaona bomba kubwa likielekea kwenye paa ya ghorofa, upesi akawaambia wenzake waelekee juu ya paa kwani mlengwa wao yupo huko.



    Basi haraka kwa kutumia ngazi wakakwea na kukwea mpaka huko juu. Wakatazama wasione kitu.



    “Atakuwa ameelekea wapi?”



    Maghorofa yalikuwa mengi sana papo. Ukiyatazama kwa juu ni kana kwamba miti ndani ya misitu. Waliwaza itakuwa mlengwa karukia maghorofa na kupotelea kusikojulikana, lakini sasa kwenda upande upi?



    “Cap, kuna suspect upande wa magharibi mtaa wa tatu. Wapo wawili wanakimbia!” sauti ilimeta kwenye kifaa cha mawasiliano cha Cap.



    Basi upesi mabwana hao wakashuka tena toka walipo waende huko wanapoelekezwa.



    Ilikuwa ni tukio la upesi sana. Hakukuwa na muda wa kupoteza. Walishuka ngazi wakiendelea kuwasiliana zaidi na zaidi.



    Walipofika chini, bwana yule mnene aliyetoa taarifa akatokea na kusimama mbele yao,



    “Subiri! Subiri!” alinyoosha mikono yake yote miwili. “Naombeni kwanza pesa yangu. Ni mimi ndiye niliwapa taarifa!”



    Mabwana hao hawakutia neno, captain alimpiga kumbo zito akadondokea kando kama kiroba, kisha wakaendelea na safari yao kwenda huko walipokuwa wanaelekezwa.



    Kulikuwa na magari mawili chini. Moja likafyatuka kuondoka kwa kasi sana. Kwa ndani lilikuwa na maafisa wawili. Wengine walikuwa wameshawahi kwenda eneo la tukio!



    Mabwana hawa wanne wakiwa wanatumia miguu, wakakimbia sana, muda si mrefu wakawasili eneo la tukio na kukuta hapo magari mawili. Moja lilikuwa ni lile lililotoka mapema zaidi na jingine ndo’ lile lililofyatuka baada ya wao kushuka chini.



    Walipotazama ndaniye, wakakuta watu wote wakiwa wamelala chini. Majeruhi wanaomimina damu lukuki!



    “Shit!” captain akalaani akibonda gari.



    “Tumempoteza mlengwa … tumempoteza mlengwa!” akanena kwenye kifaa chake cha mawasiliano kabla hajakitupa kunining’inia kifuani.



    **



    "So uko wapi? Akauliza Danielle. Uso wake ulikuwa umeparamiwa na hofu kiasi. Baada ya punde akanyanyuka upesi na kufuata gari yake.



    Majira yalikuwa ni jioni ya mapema.



    Alijikwea kwenye gari na kuelekea mahali anapopajua yeye kichwani. Aliendesha kwa kasi sana na baada ya kama dakika arobaini na tano akawa amefika kwenye eneo tulivu, hapo akaegesha gari na kuangaza.



    Ilikuwa ni katikati ya jiji pia. Hakuwa anajua atakuwapo hapo kwa muda gani. Alitazama 'side mirrors' zake kuhakikisha usalama, punde akaona gari moja likijiegesha nyuma kwa mbali kidogo.



    Hakulitilia maanani, magari kadhaa yalikuwapo hapo. Akaendelea kuangazaangaza akiwa anajiuliza. Punde akatumiwa ujumbe, "nakuja!"



    Alipotoa macho yake kwenye simu akamwona mtu karibu na gari, punde mtu huyo akafungua mlango na kuzama ndani. Alikuwa ni Marshall!



    Alikuwa anahema kwanguvu akiwa ameshikilia mkono wake wa kushoto chini kidogo ya kiwiko.



    "Twende!"



    Danielle akatia moto na gari likahepa.



    "Tuwafuate!" Alisema mwanaume ndani ya gari. Gari lile ambalo lilipaki nyuma ya mbali ya la Danielle. Kumbe walikuwa wanamfuatilia mwanamke huyo.



    "Hamna haja ya kuwafuata," akasema mwingine. "Tulichokuwa tunakitafuta, tumekipata."



    Ndani ya gari hilo alikuwa ameketi bwana James na Smith. James alikuwa amekalia usukani huku mwenzake akikaa pembeni yake.



    Bwana James alikuwa ameshikilia kamera ambayo anaipekua kutazama picha zake. Kwenye picha hizo Marshall alikuwa anaonekana akitazama chini akitembea mpaka alipozama kwenye gari.



    James akatabasamu.



    "Hatimaye. Marshall na Danielle!"



    Kisha akacheka cheko kubwa na kumtazama Smith aliyekuwa amekaa kando.



    "Sasa umenielewa sio?"



    "Hakika!"



    "Nilikuambia tuliza munkari. Ile ishu ilivyotangazwa, tumuwahi na tumtazame Danielle. Yeye atatupa ramani wapi twende."



    Smith akasafisha koo. "Lakini tulikuwa tumeshamaliza kila kitu. Mbona tukawaacha waende?"



    "Smith!" James akaita. "Mimi ndiye nimekupanga katika yote haya. Najua ninachokifanya. Trust the process. Hamna haja ya kutumia nguvu sana. Tutaharibu."



    Kukawa kimya kidogo.



    "Mbu akitua kwenye korodani, utaelewa si kila jambo lahitaji nguvu," akahitimisha James kabla hajawasha gari na kuondoka huku Smith akiwa hoi kwa kucheka.



    Maneno ya James yalimkuna.





    **



    Saa mbili usiku ...





    Marshall alibandua bandeji aliyokuwa nayo mwanzoni kisha akaiweka kando na kupachikwa nyingine na Danielle. Wote walikuwa wamekaa kwenye kiti kimoja ingali Jack akiwa amejitenga kidogo.



    Yeye alikuwa ameketi kwenye kiti kingine uso wake ukiwa umemezwa na mawazo. Alikuwa anatazama chini muda wote.



    Kichwani mwake alikuwa anatafakari mambo kadhaa, haswa kumhusu Kelly ambaye mbivu zake ametoka kuzifahamu muda si mwingi toka kwa Marshall.



    "Nilikuwa mpumbavu sana," akasema kwa sauti ya chini. Kauli yake hiyo ikafanya wote wamtazame. "Niliruhusu mapenzi yakawa upofu. Nakiri kukosa, nisameheni."



    "Usijali, Jack," Marshall akamsihi. "It's not a big deal. Kingetokea tu."



    "Hapana!" Jack akakanusha. "Nilipaswa kuhusisha akili yangu kwenye hili."



    "Nafahamu. Haukupata muda wa kutulia tangu uachane na Vio. Ulifanya maamuzi kwa upesi."



    "Ni kweli. Moyo wangu ulihitaji kupoa kwa upesi, matokeo yake ukaumizwa zaidi!"



    Kukawa kimya kidogo. Danielle alimalizia kumfunga Marshall bandeji mwanaume huyo akajiveka nguo yake vema kuficha kifua.



    "Kelly si mwanamke wa kawaida," akasema Marshall. "Ni mwanamke mwerevu, mwepesi wa kufanya maamuzi. Lakini pia mwenye uwezo wa kupambana."



    Aliposema hivyo akaweka kituo. Alikuwa anavuta kumbukumbu fulani.



    "Nimeshindwa kumweka nguvuni. Polisi waliharibu kila kitu. Badala ya kufanya kilichonipeleka, nikabaki kufanya namna ya kutoroka salama.

    Na pengine nilimshusha sana adui wangu. Sikutaraji."





    **





    Lakini kwanini Kelly alikuwa anayafanya yote hayo? Kuwafuatilia wakina Marshall na washirika? Hawakupata majibu lakini waliamini kabisa kuwa mabwana hao ndio ambao walikuwa wanafanya yale mauaji na mashambulizi ambayo bwana Ian alikanusha kuhusika nayo.



    Ikiwamo yale mauaji ya bwana O’neil na hata pia majaribio ya kumuua miss Danielle.



    “Yatupasa kulianika hili gazetini?” akauliza Danielle.



    “Hili la Kelly?” Marshall akauliza.



    “Ndio. Ama unawaza nini?”



    “Hatuna ushahidi lakini. Ni makisio tu ambayo bado hayajathibitishwa.”



    “Kwahiyo tuachane nalo?”



    Marshall akanyamaza kwanza kufikiri. “Pengine tukiandika kuhusu ule mlipuko pekee. Unajua hilo limekuwa ni jambo kubwa na mpaka sasa halijapatiwa majibu.”



    “Ni kweli.”



    Basi baada ya kujadili hilo wakapumzisha akili zao kwa kuteta mengine. Ilikuwa ni siku ndefu, hususani juma refu, haikuwa mbaya kama wangejipongeza hata kidogo.



    Danielle akaendea jokofu na kutoa chupa kubwa mbili za whiskey, akaziweka mezani na kuongezea glasi tatu ndogo nene. Kila glasi akaijaza na kumpatia muhusika.



    Na kusindikizia vinywaji vyao wakawasha na muziki kwa mbali. Basi taratibu wakiwa wanateta, taratibu wakawa wanakunywa. Kila muda ulivyokuwa unaenda watu wakazidi kuchangamka zaidi, haswa Marshall.



    Hakuwa na kichwa cha pombe. Si mzoefu wa kutia kilevi mdomoni. Kichwa chake kilianza kuwa kizito na mdomo kuwa mwepesi.



    Alikuwa anacheka kwa jambo dogo. Alikuwa amechangamka sana kiasi kwamba Jack na Danielle wakawa wanakonyezana kwa siri kumhusu mlengwa wao.



    Ilifikia kipindi Marshall akashindwa kabisa kujibeba, akaketi akinywa na kunywa. Macho yake yakaanza kumlaghai kwa kumwona Danielle ni mrembo zaidi ya anavyoonekana. Alimkumbatia mwanamke huyo mara kwa mara na kumbusubusu akimtaka wacheze pamoja.



    “Marshall, nini shida?” Danielle akauliza akimtazama mwanaume huyo machoni. Mwanamke huyo alikuwa amelegeza macho na kinywa. Alikuwa teketeke.



    Mkono wa Marshall uliminya kiuno cha Danielle na kumsogeza karibu. Marshall akamtazama Danielle kwa kitambo kidogo kabla hajasema, “unataka kujua shida yangu?”

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    “Ndio, nataka kujua,” Danielle akasema akitabasamu kwa mbali. Ni kama vile alikuwa anamsanifu Marshall.



    “Nataka nikukumbatie hivihivi siku nzima.”



    “Kweli?”



    “Ndio. Kwani kuna shida?”



    “Hapana, hamna. Lakini naogopa.”



    “Nini unaogopa?”



    Danielle akamtazama Marshall machoni akiwa kimya kidogo.



    “Naogopa maana hautaweza kuvumilia kwa muda.”



    Marshall akatabasamu. Kidogo akacheka na kumminya Danielle kiunoni. Kabla hajasema kitu akamvuta mwanamke huyo na kumbusu shingoni kisha shavuni na kwenye lips.



    “Naweza kuvumilia vinavyovumilika,” Marshall akanong’oneza. Sauti yake nzito ikasisimua mwili wa Danielle. Mwanamke huyo alihisi chuchu zake zimesimama na kuna kitu kimecheza ndani ya nguo yake ya ndani.



    “Marshall,” Danielle alitokwa na sauti pasipo kutarajia. Mwili wake ulipigwa na mtetemeko fulani wa kupumbaza. Alimtazama Marshall kisha akatabasamu kwa mbali.



    “Kwani utashindwa kuvumilia?”



    Marshall akanyoosha mikono yake kudaka makalio ya Danielle, akayapapasa makalio hayo na kuyaminya. Alafu katika namna ya nguvu, akambeba mwanamke huyo.



    Danielle alizungusha miguu yake kwenye kiuno cha Marshall, wakatazamana kimapenzi na taratibu wakaanza kusogeana wapate kukutanisha midomo. Kabla hawajatimiza adhma, Jack akasafisha koo.



    “Jamani, sijaondoka. Bado nipo hapa.”



    Marshall na Danielle wakatabasamu. Marshall akamshusha Danielle chini kisha kila mmoja akashika glasi yake na kuendelea kunywa. Wakanywa na kunywa zaidi kiasi kwamba hata Danielle akaanza kushinwa kujimudu.



    Alijikuta mwili wake unapata joto na kujawa na hamu kila anapomtazama Marshall. Jack alipoona hali inazidi kuwa tete, akaaga aende zake chumbani huku akiwa amebebelea chupa kubwa ya kinywaji.



    Ni yeye peke yake sasa ndo’ alikuwa anajitambua. Alitembea kwa kujiweza mpaka chumbano ambapo huko akajitupia kitandani na kutazama dari kwa mawazo.



    Yeye alikuwa peke yake. Hakuna mtu wa kumpa kampani mbali wala karibu. Alijihisi uchungu. Alitikisa kichwa chake mara kwa mara akiwa anaminya na kubinua lips zake.



    Akiwa katikati ya mawazo, akajikuta anakumbuka kuwa humo chumbani hakuwa mwenyewe. Hakuwa na sababu ya kuhuzunika.



    Alitazama kando yake akaona chupa kubwa ya kinywaji. Akatabasamu. Akaivuta chupa hiyo na kuikumbatia kwanguvu.



    “Nashukuru upo hapa.”



    Akafungua chupa hiyo na kunywa kana kwamba mtu mwenye kiu kupita kiasi. Alikuwa anataka kujipumbaza. Alikuwa anataka akili yake ipotee kabisa kwenye ulimwengu usiofahamika. Ulimwengu ambao haumpatii msongo wa mawazo.



    Huko sebuleni, Danielle alimbusu Marshall na kisha akamkumbatia kwanguvu. Macho yao yalikuwa yamelegea haswa, miili yao ilikuwa imepata joto.



    Hawakukaa muda mrefu hapo wakabebana kwenda chumbani. Kama watu waliojawa na uchu, wakavuana nguo na kuzitupia huko! Walivuana kwa upesi kana kwamba wanawahi kuzima bomu.



    Walipomaliza, wakanyonyana ndimi zao na kupapasana kwa fujo. Haikuchukua muda wakatimiza adhma zao na kulala usingizi mzito. Walikuja kuamka majira ya saa tatu asubuhi wakiwa hoi na wachovu.



    Ni Marshall ndiye ambaye alimwamsha Danielle.



    “Hey, muda wa kazini,” Marshall alisema kwa sauti ya chini. Danielle alifungua macho yake kivivu kisha akayafumba tena. Alikuwa anahisi kichwa kizito kama ndoo iliyojaa maji. Pia mwili ukiwa mchovu kupita kiasi.



    “Danielle, amka. Hauendi kazini?” Marshall aliita tena, mara hii akiwa amekaza sauti. Danielle akanguruma tu kunung’una lakini asifunue macho. Kope zilikuwa nzito haswa. Kila alipokuwa anataka kuzifungua zilimshinda nguvu.



    “Mimi siee --- n,” Danielle alisema kwa sauti ya puani.



    “Kwanini huendi?” Macho ya Marshall yalikuwa mekundu haswa na legevu. Hata shingo yake haikuwa inaweza kubeba kichwa, ilielemewa.



    Mwanaume huyo alipoona Danielle hajali anachokiongea basi akanyanyuka na kwenda zake bafuni. Huko akaoga na kurejea kitandani kumkuta Danielle. Bado mwanamke huyo alikuwa hajiwezi akikoroma.



    Alijaribu tena kumwamsha lakini wapi, mwisho wa siku hata na yeye akalala. Walikuja kuamka majira ya saa saba mchana. Mara hii Danielle ndo akimwamsha Marshall.



    “Amka ni mchana sasa.”



    Chakula kilikuwa tayari mezani. Marshall alijisogeza kwenda huko akamkuta Jack. Wakala wakiwa kimya kidogo kana kwamba hakuna kilichotokea jana yake. Ni kama vile kila mtu alikuwa anamtegea mwenzake.



    “Nimekuta missed call za James,” Danielle akavunja ukimya.



    Marshall akamtazama, “Anasemaje?”



    “Ametuma ujumbe,” Danielle akajibu na kuongeza, “Anasema ananihitaji tuonane. Ni kikao muhimu.”





    **





    *SEHEMU YA 31*





    Marshall alimtazama Danielle pasipo kusema jambo. Alitafuna na alipomeza akajifuta mdomo wake na kusema, “hajakuambia maudhui ya kikao hicho?”



    Danielle akabinua mdomo. “Lah! Hajaniambia. In fact, sijataka kumuuliza. Alin’tumia ujumbe baada ya kuona sijapokea simu zake.”



    “Inabidi uwe makini, Danielle,” Jack akatia neno. Alikuwa anatafuna akiwa anamtazama mwanamke huyo. “hawa watu wa usalama, ni wa kuishi nao kwa umakini.”



    “Najua. Najua ananitafuta sana lakini hawezi nipata,” Danielle akatia neno. Basi wakala mpaka kikomo, mwanamke huyo akanyanyuka na kwenda kujiandaa aende kazini.



    Kitendo cha kunyanyuka hapo, Jack akamtazama Marshall kisha akatabasamu. Marshall hakusema jambo, akaendeleza kula kana kwamba hakumwona Jack.



    Jack akatabasamu. Alikuwa anaendelea kumtazama Marshall.



    “Oyah … oya Marshall,” Jack akaita kwa sauti ya chini. Alipoona Marshall haitiki, akamgusa mkono. “si nakuita ndugu.”



    “Unataka nini?”



    “Mbona hasira mzee?” Jack akauliza kisha akatabasamu na kulegeza macho, “Vipi jana mwanangu?”



    “Sikumbuki!”



    “Aaah ukumbuki wapi wewe!”



    “Niambie basi mwanangu. Ilikuaje? Eeenh? … oyaaa … niambie basi mwanangu? … najua ilikuwa fresh kweli!”



    “Sasa kama unajua hivyo kwanini unauliza?”



    “Si nataka tu kuhakikisha kwa kinywa chako.”



    “Mimi sina chochote cha kukuhakikishia.”



    “Natak ---”



    Danielle akafika sebuleni. Jack akaacha kuongea na kubaki akitafuna.



    “Kwaherini, guys. Baadae!”



    Mwanamke huyo akambusu Marshall kisha akaenda zake. Jack akamtazama tena Marshall na akashinda kujizuia kutabasamu.





    **



    Saa nane mchana …





    “Nipo hapa ku make a deal na wewe,” alisema bwana James akimtazama Danielle machoni. Bwana huyo alikuwa amevalia suti yake maridadi rangi nyeusi. Alikuwa yu mwenyewe, bwana Smith akimuacha kwenye gari.



    Ingawa Danielle hakuwa anajua ni nini bwana James alikuwa amefuata, lakini alijikuta akiwa kwenye lepe la mashaka. Alikuwa anahisi kuna kitu hakipo sawa. Alijikuta anawaza mambo kadhaa kichwani mwake akipembua na kuchambua wapi atakapokuwa amekosea.



    “Unajua bwana Ian alikutwa akiwa amenyweshwa kiasi kikubwa cha kilevi, Sodium thiopental, hivyo nachelea kuamini kuwa bwana huyo atakuwa ametoa taarifa mahali. Taarifa ambayo nasi tunaitafuta kwa udi na uvumba.



    Imekuwa ni ngumu, hataki kusema wala kushirikiana nasi. Lakini najua wewe utanisaidia kwenye hilo.”



    Danielle akatikisa kichwa, kabla hajatia neno akaona bahasha ikitupwa mezani.



    “Pengine ukiona hayo utabadilisha mawazo yako,” alisema bwana James.



    Danielle akavuta bahasha na kuitazama kwa ndani. Mulikuwa na picha. Alipozitama picha hizo akajikuta akipoteza nguvu. Akitetemeka.



    Alimwona Marshall pichani akiwa anajipaki kwenye gari lake. Jana tu, punde alipoenda kumchukua bwana huyo.



    “Vipi hapo Danielle?” bwana James akauliza akitabasamu.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    “Ni nini unataka, James?”



    “Nimeshakuambia ninachotaka. Taarifa za bwana Ian.”



    Danielle akanyamaza akimtazama bwana huyo.



    “Deal?” James akauliza.



    Baada ya muda kidogo James akatoka ndani ya ofisi hiyo kwenda kukutana na mwenzake ndani ya gari. Alipoketi akatabasamu. Alikuwa na furaha sana kwani hatimaye alikuwa amewaweka mtegoni watu waliokuwa wanamsumbua.



    “Kwahiyo?” Smith akauliza.



    “Nimeshaelewana naye, usijali,” bwana James akamtanabahi.



    “Utawaacha huru? Inabidi wakamatwe!”



    “Ah ah! Nilishakuambia hapo kabla. Tulia. Tulia. Najua cha kufanya.”



    “Lak--”



    “Smith, ukiendelea hivi nitajitoa muda si mrefu.”



    Hiyo ikawa kauli ya mwisho ya bwana James kabla hajawasha gari na kutimka.





    **





    Saa kumi na moja jioni ...





    Kilikuwa ni kikao cha siri. Hakukuwa na watu kabisa hapa isipokuwa wawili tu ambao ni Abdulaziz na Jamal. Manwana hao walikuwa wameketi kwenye chumba wakiwa wamekunja nne na kujinywea mvinyo mweupe.



    Abdulaziz alikuwa amevalia kanzu nadhifu rangi ya maziwa ilhali Jamal yeye alikuwa amevalia sare zake za jeshi. Nguo nyeupe zenye vielelezo vingi vya vyeo. Lakini pia safi zinazong'aa.



    Vidoleni mwa Jamal kulikuwa na pete mbili za dhahabu. Na saa iliyokuwa mkononi mwake ilikuwa ni ya Rolex, kubwa na ya aghali. Vilevile kwa Abdulaziz. Saa yake ilikuwa imedariziwa na dhahabu.



    Kama tu ungelipata saa hii, basi shida zako ndogondogo zingekoma mara moja.



    Uso wa Jamal ulikuwa mwembamba, pua ndefu na mdomo mwekundu. Mustachi wenye afya na kidevu kisafi kilichopruniwa ndevu.



    Macho yake yalikuwa makubwa yenye kiiini kikubwa cheusi. Sauti yake ilikuwa nyembamba kali.



    Maongezi haya hayakuwa yameanza hapa karibuni, lah! Yamedumu kwa kama lisaa. Huko nje walikuwa wamesimama wanajeshi imara wenye silaha zao.



    "Kwahiyo unasemaje?" Abdulaziz akauliza. Jamal akashusha pumzi ndefu kisha akanywa fundo moja la mvinyo wake. Akasafisha koo na kusema, "nipe leo, nitakuletea kichwa chake usiku huu!"



    "Uhakika?" Abdulaziz akauliza.



    "Ndio. Nakuhakikishia," Jamal akasema kisha mabwana hawa wakapeana mikono ya makubaliano.



    Waliteta mengi. Na huyo ambaye kichwa chake kilikuwa kinaenda kuvunwa alikuwa ni wa kwanza kati ya wengi wanaofuata.



    Damu itamwagika.



    Bwana Jamal akaenda zake ambapo ndani ya muda mchache, kama lisaa moja, akawa amekutana na wanaume wanne. Wanaume wa kazi. Wanaume hao akawapa maelekezo lakini pia na deadline.



    Anataka kichwa cha mtu usiku huu.



    **





    Nani angedhani usi huu ungeleta shari? Hakuna. Upepo ulikuwa unapuliza na watu, wengi wao, walikuwa wameshajiweka kwenye maskani zao kujipumzisha.



    Wazazi na watoto wao wakiwa wamejumuika kwenye meza kula. Wengine wakiwa wamekaa nje vibarazani ama huko mjini wakirandaranda kibiashara.



    Lakini kwenye muda kama huu kwa ujumla kulikuwa ni kimya. Maeneo mengi yalikuwa yamemezwa na ukimya lakini pia na kiza. Kama kuna mwanga basi ni zile za nje, za ndani zimepumzishwa watu wakiwa wamefumba macho yao kupumzika.



    Lakini sio wote. Mabwana hawa takribani wanne waliokuwa wamevalia kombati nyeusi za kazi walikuwa tayari wapo kwenye lindo. Mikono yao imebebelea bunduki na nyuso zao zimefunikwa kwa barakoa nyeusi za mipira.



    Walikuwa ni makomando. Na usiku huu walikuwa na kazi moja tu, kumuua Marietta, kisha mwili wake ukateketezwe na kichwa chake kihifadhiwe na mtoto wa mfalme Abdulaziz.



    Hapa walipokuwa wamesimama ilikuwa ni kama robo kilometa tu kufikia makazi ambapo wanaamini Marietta yupo. Basi kwa kufanya ufanisi, mabwana hawa wakajigawa, wawili waende mashariki na wawili waende magharibi kisha wakakutanie mahali pa tukio.



    Wakiwa wanafanya vivyo, wawe wanawasiliana kujuzana kinachoendelea.



    Basi wanaume wawili wakatembea kwa tahadhari mpaka karibu kabisa na makazi ya Mahmoud. Wakawasiliana na wenzao na yote yalikuwa sawa. Nao muda si mrefu wakawa wamefika eneo la tukio wakiwa salama salmini.



    Wakatazamana na kisha kiongozi wao akaamuru wawili waende nyuma ya jengo na wawili wabaki kwa mbele ili kuzuia kutoroka kwa mlengwa. Walipofanya vivyo, wanaume wale wawili wakatumia pini maalumu kutengulia vitasa vya mlango alafu wakazama ndani wakiwa wamebebelea kila aina ya tahadhari.



    Bunduki zilikuwa mbele na macho yakiwa yanaruka na kuambaa-ambaa huku na kule. Kulikuwa ni kiza, lakini si kile totoro, lah! Kiza cha kuweza kuona hata panya akikatiza.



    Wakapita sebuleni, wakaendelea kusonga, mpaka kufika chumbani. Chumba cha kwanza kabisa wakakifungua, lakini katika namna ya ajabu wakakumbana na moshi mzito haswa.



    Ilikuwa kosa wao kuvuta hewa hiyo. Walijikuta wanakohoa kwanguvu na kwa kufululiza kiasi kwamba hata kushikilia silaha zao ilikuwa haiwezekani.



    Wenzao walioko nje waliposikia hayo, upesi wakafanya namna kwenda kukuta wenzao lakini kwa tahadhari hawakusonga ndani. Walishatambua ni sumu. Basi wasiwe na namna wakawatazama wenzao wakiwa wanateketea.



    Mmoja wao akiwa anakohoa na kutetemeka, akawakimbilia wenzake kana kwamba mwehu. Macho yake yalikuwa yamebadilika rangi, yamekuwa ya kijani.



    Mdomo wake ulikuwa mkavu kupita kiasi mpaka kupasukapasuka. Ulimi wake nao ulikuwa mkavu kama tambara bichi lililokakamazwa na mwanga mkali wa jua.



    Haikujulikana hata ni muda gani alivua barakoa yake. Hakikuwa kitu cha kuambiwa, alikuwa anapitia maumivu makali. Nguo ambayo ilikuwa imembana hapo awali, ilikuwa sasa imepwaya!



    Hakudumu muda mrefu, akadondoka chini akiwa na mwili kama uji! Akafa kifo cha ajabu kabisa.



    Hata baadae hewa ya sumu ilipoambaa, wakaenda kumkuta mwingine ndani, kiongozi wao, akiwa amerojeka vibaya mno angalau ya yule aliyekimbilia nje.



    Basi wanaume hao, wawili waliobaki, wakatoa taarifa kwa mkuu wao Jamal kuhusu walichokutana nacho. Wameshindwa kumpata muhusika na zaidi wamepoteza wapambanaji wawili!



    Taarifa hizo zikamfikia pia na Abdulaziz asubuhi na mapema. Akaumwa sana na kukasirika. Hata mke wake akalazimika kukaa naye mbali. Mwanaume huyo alijiwazia wapi atakapokuwepo Marietta. Wapi atakapokuwepo Mahmoud?



    Alitaka kuonana na Jamal haraka iwezekanavyo.



    Jamal akiwa amepaliwa na hofu, akafika nyumbani kwa Abdulaziz upesi kwenye majira ya saa tatu. Akamkuta Abdulaziz akiwa amefura, ameweka kahawa yake kwenye kikombe lakini hajainywa mpaka imepoa.



    Uso wake ulikuwa mwekundu, macho yake ameyakodoa na ndita amezikunja. Hata Jamal alifahamu mambo yalikuwa yameenda kombo. Abdulaziz hakuwa na msalia mtume kwenye njia yake ya kwenda ufalmeni. Alikuwa anaona anakawia.



    “Nini kimetokea??” akafoka Abdulaziz. Alikuwa anamtazama Jamal kana kwamba ni mtu mkaidi. “Uliniahidi nini Jamal?”



    “Najua, mkuu lakini haikuwa vile ambayo tumetarajia.”



    “Jamal!” Abdulaziz akaita. “Hakuna kitu chochote cha kutaraji katika ulimwengu huu bali unakitengeneza.”



    “Najua. Kila kitu kilikuwa kimepangwa lakini adui yetu ni kama alikuwa anatutaraji kwani alishapanga mipango yake. Mitego ya sumu ilikuwa imewekwa ndani ya vyumba vyote. Tena sumu kali kupita kiasi.”



    Abdulaziz akafikiria kwa muda kidogo kabla hajatikisa kichwa chake na kusema, “Mahmoud!”



    Akanyamaza tena kidogo akikuna kidevu.



    “Ni Mahmoud,” akatia neno akitazama chini. Alikuwa anafahamu fika kuwa bwana huyo, yaani Mahmoud, ni mtaalamu haswa wa mambo hayo ya utengenezaji wa sumu kwakuwa mbobevu kwenye taaluma ya kemia.



    Kwenye mambo mbalimbali aliwahi kumtumia bwana huyo na kumpa matokeo chanya. Ikiwemo pia kwenye misheni ya kumpoteza Raisi wa Marekani.



    Kwenye misheni hiyo bwana Mahmoud alitumia taaluma yake kutengeneza gesi kama kilevi ambacho kilitumika kumziraisha Raisi mara moja punde tu alipovuta.



    “Sasa tunafanyaje?” Jamal akauliza . abdulaziz akafikiria kidogo kabla hajasema, “Najua mahali Mahmoud alipo.”



    Kisha akamtazama Jamal.





    **



    Saa yake ya mkononi ilikuwa inasema ni saa sita mchana. Alimalizia kunywa juisi yake kisha akalipa na kunyanyuka kutoka ndani.



    Alitazama kushoto na kulia. Alikuwa yu sawa, alitengenezea koti lake mwilini alafu akaendelea na safari.



    Mwanamke huyu alikuwa amebana nywele zake vema na macho yake ameyafunika kwa miwani rangi nyekundu ya kufifia. Mwendo wake ulikuwa wa kiukakamavu utadhani hajavalia viatu vya visigino virefu.



    Alipotembea kwa muda kidogo akatoa pipi ya kijiti na kuimumunya. Alitembea kwa kama dakika nne kabla hajachoropoa simu yake na kuwasiliana na Marietta.



    “Unakuja lini?” lilikuwa swali la kwanza. Kelly akachomoa pipi yake mdomoni.



    “Muda si mrefu, madam. Passport ipo ndani ya makazi yangu. Unajua siwezi kusafiri pasipo kuwa nayo.”



    “Haitakuwa imebebwa?”



    “Hapana! Niliweka sehemu ya siri. Hakuna mtu anayeweza kuibaini isipokuwa mimi pekee.”



    “Sawa. Utakapoipata, angalia kama kuna uwezekano wa kupata ndege yoyote ya mapema, hata kama ni ya leo. Sawa?”



    “Usijali.”



    Kelly akarejesha simu yake mfukoni na kuendelea kuchapa mwendo.





    **



    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    SEHEMU YA PILI …





    Baada ya mwendo wake kutimiza dakika kumi na tano, mwanamke huyo akazama ndani ya jengo moja ghorofa. Halikuwa lile la makazi yake, lah! Lilikuwa ni jingine ambalo lilikuwa limechoka kidogo.



    Humo akapandisha ngazi mpaka juu kabisa kwenye paa. Akavua viatu vyake na kurukia ghorofa la kwanza kisha akasonga na kurukia ghorofa la pili. Alipokuwa huko juu, akavua koti lake na kuligeuza. Lilikuwa na rangi nyingine.



    Kwa kulitazama upesi ungelidhani ni jingine.



    Basi akashuka kwenye ghorofa hilo na punde, akashika chumba fulani kisicho na tija, humo akapanda juu na ndani ya muda mfupi akashukia ndani ya chumba chake.



    Japo mwanamke huyo alikuwa amevalia viatu vya visigino virefu, sauti haikutoka hata punje. Kila kitu kilikuwa kimya kimya.



    Basi akaendea chumbani, huko akapenyeza mkono wake nyuma ya kabati na kupapasapapasa. Kidogo akashika kitu, akakivuta na kukitazama. Kilikuwa ni karatasi. Akashangaa. Hakuacha karatasi hapo.



    Alipofungua karatasi hiyo akakutana na ujumbe ulioandikwa kwa marker pen nyekundu.



    “Vitu vyako ninavyo. Nitafute.” baada ya ujumbe huo kulikuwa na namba za simu kwa chini.



    “Shit! Shit! Shit!” Kelly akalaani kwa herufi kubwa. Alishika nywele zake kwanguvu akizinyongorota. Alipatwa na msongo wa mawazo upesi. Alianza kuhisi anawehuka.



    Akarudi tena nyuma ya kabati na kupapasa, kweli hakukuwa na kitu! Inawezekanaje?



    Tukio hilo likamfanya mwanamke huyu afanye ukaguzi wa eneo lake. Na asitafute sana akajikuta akiuona mwili wa mtu nyuma ya kochi. Alipoutazama mwili huo vema akagundua ni wa afisa polisi.



    Kidogo akauona tena mwili mwingine. Ulikuwa unafanana tu na huo wa kwanza. Mwanamke huyo akajikuta akishusha pumzi ndefu.



    Haraka akaendea glovu chumbani mwake kabatini, akajiveka na kuipima miili hiyo kwa mkono. Bado ilikuwa hema. Bado ilikuwa hai! Akastaajabu na hili. Mabwana hao wawili walikuwa wamepoteza fahamu wakiwa kwenye usingizi mzito sana. Hata mapigo yao ya moyo yalikuwa yanapiga kwa mbali.



    Nani aliyewaziraisha?



    Akaketi akiwaza. Aliyewatenda hao maafisa ndiye ambaye amebeba vitu vyake. Amejuaje kama vipo kule? Na kwanini avibebe?



    “Marshall,” Kelly akajikuta akisema kwa sauti ya chini. “Ni Marshall. Hakuna mwingine!” upesi akatoa simu yake na kupiga zile namba, baada ya muda kidogo, simu ikapokelewa na sauti ya kiume.



    “Naona umepata ujumbe wangu. Sasa njoo kwenye anwani ntakayokutumia,” sauti ikasema na kisha simu ikakata.



    Kelly akatikisa kichwa.



    “Nini hiki?”



    Kidogo akasikia sauti za watu huko nje. Akashtuka. Alitupa macho yake ya tahadhari mlangoni.



    Huko nje kulikuwa kuna maafisa wawili wa usalama. Maafisa hao walikuwa wamebebelea vikombe vya take-away vya kahawa. Walifungua mlango na kuzama ndani. Kelly alikuwa tayari ameshapotea!



    Ni punde, wakaona miili ya wenzao chini.





    **



    “Serious?”



    “Ndio, serious!” Kelly akasema akiwa anatembea. Mwendo wake ulikuwa ni wa haraka. Alikuwa anatazama nyuma mara kadhaa. “Sijajua nifanyeje? Anataka kuonana na mimi!”



    Kukawa kimya.



    “Nifanyeje?” Kelly akauliza. “Nime stuck kabisa. Kichwa kimegoma.”



    “Nenda kaonane naye.”



    “Serious?”



    “Hakuna namna. Nenda kamskize anasemaje.”



    Basi Kelly akakata simu na kutekeleza kile ambacho ameambiwa. Akatuma ujumbe kwenda kwenye ile namba kwamba yu njiani anakuja.



    Kidogo akajipaki kwenye usafiri kuanza safari.





    **



    Alasiri …





    “Kelly, mimi sina mengi sana ya kujua toka kwako isipokuwa yale maswali yangu ya mwanzoni,” aliema Marshall akimsogezea Kelly glasi ya maji. Eneo lilikuwa limetulia na watu wako tenge. Macho ya Marshall, Danielle na Jack yote yalikuwa yanamtazama Kelly.



    Mwanamke huyo alikuwa ameketi kwenye kiti cha peke yake akiwa amekunja nne. Japo mwili wake ulikuwa umetulia, moyo wake ulikuwa unakita bum-bum-bum-bum kifuani.



    “Naomba unikumbushe maswali hayo,” akasema Kelly.



    “Sawa. Labda niyageuze na kuyafanya yawe ya moja kwa moja zaidi,” akasema Marshall na kuuliza, “Unamfanyia kazi nani?”



    Kabla Kelly hajajibu swali hilo, simu yake ikaita. Alikuwa ni Marietta. Alipokea simu hiyo na kuiweka sikioni.



    “Umefika?”



    “Ndio.”http://pseudepigraphas.blogspot.com/



    “Naomba niongee na Marshall.”



    Kelly alidhani amesikia vibaya. Marietta akarudia tena ombi lake. Anataka aongee na Marshall.



    Basi Marshall akapewa simu.







    MWISHO WA MSIMU WA 3

    ENDELEA KUFUATILIA MSIMU WA 4



    MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Blog