Search This Blog

Sunday 20 November 2022

MSAKO WA HAYAWANI - 2

 





    Simulizi : Msako Wa Hayawani

    Sehemu Ya Pili (2)







    "Karibuni." Mzee Maliki aliwakaribisha. Alikuwa mtu wa makamo alietazamia kustaafu muda wowote. Sare yake ya Ukamishna Msaidizi ilimpendeza sana. Ofisi yake ilikuwa pana na nadhifu.

    "Ketini." Wakaketi. "Ni nani mwenzako Bessy?"





    "Luteni Dennis Makete. Baba yake, Dk.Raymond Makete, aligongwa na gari leo asubuhi nyuma ya Benki ya Wakulima. Aliemgonga hakusimama na hakuna mtu aliwahi kuzisoma namba za gari. Tunaamini mtu huyo ni Kassim Hashir na alimgonga Mzee Makete kusudi."

    "Simkumbuki..."





    "Ulimfungulia faili hili mwaka 1969 na kulifunga mwaka 1974, ukiamini amekufa."

    Mzee Maliki akalipokea lile faili na kulifungua. Baada ya kuupitisha macho ukurasa uliokuwemo, akasema, "Ndiyo, nakumbuka sana. Nilipokea telegram kutoka Polisi ya Kenya ikieleza Kassim Hashir alifikwa na ajali mbaya ya gari na kufariki papo hapo. Sijui kwa nini telegram hiyo haimo humu! Ukweli ni kwamba kesi yake ilikuwa dhaifu sana. Kila mtu aliidharau, pamoja na kuhusiana na mamilioni ya pesa za kigeni. Kwa nini mnadhani yuko hai na ndiye aliemgonga Dk.Makete?"





    "Mzee Makete alizinduka kwa nukta chache alipokuwa thieta na kulitaja jina lake."

    "Hawezi kuwa amekosea?"

    "Hatujui. Lakini kwa vile hatuna fununu yoyote nyingine..."

    "Ikoje hali ya babako, Denny?"

    "Niliarifiwa amejeruhiwa vibaya. Lakini Dk.Beka anaamini hayuko katika hali ya kutisha." Alijibu Denny. "Huwezi kufanya chochote kile kuhusu mtu huyo?"





    " Hatujui chochote kile zaidi ya kulijua jina lake na kuiona picha iliyomo humo, ambayo sidhani kama itatusaidia sana,ni ya zamani mno - tuko gizani kabisa."





    "Mmmh, labda nianze toka mwanzo." Alisema Mzee Maliki, akiwaza. "Kama unavyofahamu, nchi hii ilipata uhuru mwaka 1960. Bwana Nelson Benjamin Nseloa akawa Rais wa kwanza. Watu wote walifurahi jinsi alivyopigani uhuru, wote tulimpenda Nselo.





    "Lakini kadri miaka ilivyozidi kupita bila ya yeye kutimiza kile ambacho wananchi wengi walitamazamia angetenda, mapenzi yakaanza kupungua. Wananchi wengi walitazamia kuwa baada ya uhuru, Nselo angewafukuza wageni wote - wazungu na waasia na mali zao kugawiwa kwa wazawa. Yeye hakufanya hivyo. Kinyume chake, aliwatetea na kuwalinda. Kwa vile tangu mwanzo walikuwa ndio wafanyabiashara wakubwa na wenye kumiliki mashamba makubwa na mazuri, wakazidi kutajirika. Wananchi wakaishiwa furaha."





    Mzee Maliki alitoa mtemba akaanza kuujaza tumbaku kabla hajauwasha na kuukoleza.

    "Mkuu wa majeshi wakati huo, Meja Jenerali Ibrahim Mbelwa,akaamua kuutumia mwanya huo. Akaipindua serikali ya Nelson Benjamin Nselo,ambaye alikuwa ng'ambo, na kutwaa madaraka."





    Baada ya kuuwasha mtemba kwa kutumia njiti tatu,akaendelea, "Hiyo bila shaka, ni historia mnayoifahamu vizuri. Inasikitishwa vile watu wanavyofurahishwa na kitendo cha Mbelwa, hasa alipowafukuza wageni na kugawa mali zao kwa wananchi. Lakini haukupita muda mrefu kabla ya hulka ya kweli ya Mbelwa kudhihirika. Kwa vile hakuwa na elimu, aliwachukia wasomi, kwa vile alikuwa Mwislam ,aliwachukia wakristo. Kwa vile alikuwa Mshongwe, aliwachukia watu wa makabila mengine,hasa kabila la Nelson Nselo. Si tu aliuteketeza uchumi wa nchi, bali aliteketeza watu karibu milioni. Kwa vile wakati huo tulikuwa miloni chache tu, idadi hiyo ilikuwa kubwa ya kutisha. Watu wakaanza kujuta."





    Mtemba ulikuwa umezimika. Akauwasha tena kabla ya kuendelea. "Kwa sababu moja au nyingine, maelfu ya wananchi wakaihama nchi na kuomba hifadhi katika nchi jirani. Nelson Nselo akaweza kuwaunganisha na kuwapa mafunzo ya kijeshi. Wakati ulipowadia wakaingia nchini. Wakashinda kirahisi askari wa Ibrahim, ambao hawakuwa na moyo hata na moyo wa kupigana. Yeye mwenyewe aliuliwa wakati akijaribu kutoroka nchi. Risasi zangu zilikuwa miongoni mwa risasi zilizomtoa roho."





    Kikapita kimya cha muda, Dennis akajikuta anamtazama Mzee Maliki kwa matazamo mpya. Mzee huyo akaendelea, "Sasa kuhusu Kassim Hashir. Yeye na Ibrahim walikuwa marafiki, licha ya kutokuwa rika moja. Akampa Kassim pasipoti ya kibalozi na kumtumia kutorosha mali. Katika kipindi cha utawala wa miaka mnne ya utawala wake, Kassim alitorosha mamilioni kwa mamilioni. Alikwenda Ulaya karibu kila wiki kupeleka pesa za kigeni na chochote kile ambacho kilikuwa mali. Kazi hiyo inasemekana aliimudu vizuri. Pia inasemekana alikuwa na kichwa cha biashara. Hakuyaacha mamiloni hayo yalale benki, aliyazalisha katika vitega uchumi mbalimbali.





    "Alipoona mambo yanaanza kuharibika hapa nyumbani, akayeyuka. Kwanza alikimbilia Ulaya, baadaye akawa hatulii mahali pamoja. Akawa mfanyabiashara wa kimataifa. Bila ya shaka aliposikia Ibrahim amekufa aliinua mikono mbinguni. Hakuwa na mtu wa kumghasi na wala kugawana nae tena. Na kama ni kweli angali hai atakuwa tajiri mkubwa sana - tajiri wa kuweza kushindana na serikali yoyote ya nchi ya Kiafrika."





    Bessy akashusha pumzi. "Sioni kitendo chake cha kurosha mali kinaweza kuhusiana na Dk.Makete."

    "Hata mimi sioni." Alikubali Mzee Maliki. Dennis akauliza, "Kwa nini ulisema kesi yake ilikuwa dhaifu - hamkujali sana?"





    "Mara tu baada ya Ibrahim kung'olewa, niliteuliwa kuongoza skwadi ya kuwasaka, kuwakamata na kuwapeleka mahakamani wote waliotenda makosa wakati wa utawala wa fasishisti huyo. Walikuwa wengi, zaidi ya elfu. Wengine walikuwa wamefanya makosa madogo tu, lakini wengi walikuwa wametenda unyama kweli kweli. Kwa wengine palikuwa na ushaidi, na kwa wengine hapakuwa na ushaidi wa kutosha. Ilikuwa kazi kubwa kupata majina yao na makosa yao kuwafungulia mafaili, kuwasaka, kuwakamata, kutafuta ushaidi na hatimae kuwapeleka mahakamani. Kadhaa tuliwanasa na walihukumiwa kunyongwa au kufungwa. Lakini wengi pia ilibidi waachiwe na makama kwa uhaba wa ushaidi."





    " Wote tuliona Kassim angekuwa mmojawapo wa kuachiwa. Kwanza, kwa vile alikuwa na pesa, angeweka mawakili kabambe. Pili, hatukuwa na ushahidi madhubuti kumtia hatiani. Mashahidi tuliowapata ni maafisa wa forodha na uhamiaji, ambao walikiri kuwa hawakuwa wakimpekua Kassim aendapo ng'ambo kwa sababu ya pasi yake ya kibalozi, ingawa walishuku mizigo yake. Huo sio ushahidi kitu mahakamani. Walishindwa hata kusema kwa hakika ni vitu gani alivitorosha.





    "Ushahidi mwingine ulikuwa wa minong'ono tu, wa watu waliokuwa wakimtafutia bidhaa,ambao hatimae akawadhulumu. Unadhani wangekubali kusimama mahakamani na kutoa ushaidi? Wao na wao walikuwa wanavunja sheria. Hata kama wangekubali ili kumkomoa Kassim,wakili yoyote yule angewachakaza vibaya sana."





    "Bessy akauliza, "Kwa hiyo hakuna juhudi zozote zilizofanywa za kutaka akamatwe huko Ulaya na kumrudisha nyumbani?"http://pseudepigraphas.blogspot.com/







    "Oh! Tuliiarifu Interpol, lakini ilikuwa ni kazi bure. Kama nilivyosema, Kassim alikuwa hatulii mahali pamoja. Na inaaminika alukuwa na pasi kadhaa za bandia. Nilipoipokea telegram ya kutoka Kenya, nilishusha pumzi na kumshukuru Mungu. Nikalifunga faili lake."





    "Unamaana ukikutana naye mitaani hutamkamata?" Bessy aliuliza.

    "Huku nikijua anatuhumiwa kumgonga Dk. Makete?"

    "Hapana kabla yake."

    "Ningemfanya nini? Hivi sasa hata hao maafisa forodha na uhamiaji, na hao waliompa bidhaa hawataweza kupatikina kirahisi."





    Dennis akauliza, "Ndio kusema inawezekana amerudi hapa nchini siku nyingi bila ya mtu yoyote kumjali?"

    "Inawezekana kabisa kama kweli angali hai. Miaka zaidi ya ishirini ni muda mrefu Denny. Watu hubadilika. Watu husahau mengi. Mimi sidhani kama nitamtambua nikimwona. Isitoshe, bila shaka atakuwa amejipa jina jingine."

    "Unazungumza kama vile unaamini kuwa upo uwezekano wa yeye kuwa angali hai?"





    "Oh, upo kabisa. Siku hizi pesa zinaweza kufanya karibu chochote kile. Zinaweza kumfanya afisa wa polisi 'aokote' kitambulisho cha Kassim Hashir ndani ya gari lililopata ajali mbaya, na aamini kwa dhati kuwa marehemu ndiye Kassim Hashir. Hilo linaweza kutendeka kokote duniani, siyo hapa Afrika tu."





    Baada ya kuukoleza mtemba kwa kuuvuta kwa nguvu, akamuuliza Bessy, "Umeshamfungulia faili?"

    "Bado. Jina lake nimelipata muda mfupi tu uliopita."

    "Nenda masjala ukamfungulie, kwa kosa la kijaribu kuua."

    "Bessy akakibali kwa kichwa. "Nitafanya hivyo."

    "Sidhani kama kuna lolote la kuongeza. Labda moja tu. Kuna mwandishi mmoja wa habari wa kujitegemea, Harold Chisimba, mbaye alisumbuliwa sana na Ibrahimu Mbelwa kwa sababu ya utafiti wake. Amekwishaandika kitabu....."





    "Nimekisoma," alisema Bessy. "Nadhani ni mtu wa kumuona. Si tu anaweza kuwa na moja au mawili ya kuwaeleza kuhusu Kassim Hashir, bali anaweza kuwa hata na picha zake nzuri zaidi kuliko hii iliyomo ndani ya faili. Alikuwa mpiga picha mzuri sana."





    "Tutampata wapi?"

    "Anaishi Wazalendo Hotel, chumba namba nne.Ana hisa kubwa katika hoteli hiyo."

    "Tutamtembelea." Alisema Bessy akiinuka. "Asante sana, Mzee Maliki."

    "Karibuni tena." Wageni wake walipokuwa wakikaribia mlango akasema kwa kusita, "Bessy, una uhakika unaitaka kesi hii?"

    "Una maana gani?"

    "Naamini ni kesi ngumu na ya kutatanisha. Kassim Hashir...." Uso akiwa ameukunja, Bessy akamkatiza.

    "Una hofu kuwa itanishinda?" Mzee Maliki akakubali kwa kichwa, macho chini.

    "Kuna kesi yoyote ambayo imewahi kunishinda?" Bado akiangalia chini akatikisa kichwa.





    "Hii ikinishinda," Bessy alisema kwa sauti kavu, "Nitajiuzulu."





    ************************************





    Kembo aliliegesha gari lake karibu nusu kilomita mbali na Tupetupe Hotel, akateremke na kuelekea kwenye hoteli hiyo kwa mwendo wa taratibu, macho yake yakiangaza kijanja kila pembe kutazama kama palikuwa na ye yote mwenye shauku naye.





    Tupe tupe ilikuwa ni hoteli yenye ghorofa nne, kukuu, iliyopendwa zaidi na wahuni. Mgahawa na baa na ukumbi wa dansi vilikuwa chini. Juu kulikuwa na vyumba vya kulala vya bei nafuu. Palikuwa na vyumba vya kitanda kimoja, vitanda viwili na hata vitanda vinne.





    Kembo aliitembelea hoteli hiyo kwa nadra kadri alivyoweza. Na kila alipoitembelea alisita kwanza kabla ya kuingia ndani ya lifti yake iliyochakaa. Aliamini kwa dhati kuwa usingepita muda mrefu lifti hiyo ingeua. Lakini wakati mwingine wazo la kuhesabu ngazi hakuliafiki hata kidogo.

    Lifti iliposimama salama na mlango kufunguka, Kembo alitoka na kwenda kwenye mlango wa chumba Namba 406. Akaugonga kwa kidole cha shahada na kusubiri kwa nukta tano. Kisha akagonga tena.





    Mlango ukafunguliwa na kijana wa miaka thelathini mwenye nywele nyingi aliyebana sigara kwenye kona ya mdomo. Uso wake umepooza lakini alipomwona Kembo ukachanua.

    "Za hapa, Chiko?"

    "Safi, Bwana Kembo." Sauti yake alikwaruza, itakayo kooni. "Karibu." Kembo akaingia mlango ukafungwa.





    Chumba hicho kilikuwa kimoja kati ya vyumba vizuri vya hoteli hiyo. Kilikuwa kidogo kipana chenye vitanda viwili, meza moja duara, viti viwili na kabati la nguo. Vijana wawili walikuwa wameketi vitini. Mmoja alikuwa mdogo kuliko Chiko, mwingine kigogo mkubwa. Mezani palikuwa na karata, pesa, chupa za pombe, paketi za sigara na kisahani cha kuwekea vishungi na majivu ya sigara. Chumba kizima kilijaa harufu ya moshi wa sigara, licha ya madirisha kuwa wazi na pangaboi juu kuzunguka.





    Baada ya kuufunga mlango na kugeuka, Chiko akasema, "Fensy, Hoza, kutaneni na Bwana Kembo." Vijana hao waliitika kwa vichwa. Walikuwa na nyuso kavu kuliko umri wao.

    Hoza aliekuwa mdogo, akainuka, akisema, "Karibu kiti Bwana Kembo." Yeye akaenda kuketi kitandani.

    "Hapana, asante," Alisema Kembo, naye akijiwashia sigara. "Sina muda. Sitaketi." akapuliza moshi na kusema, "Chiko, umefanya kazi nzuri. "Umewezaje kupata habari kamili vile, tena katika muda mfupi tu?"





    "Dadangu ni Nesi."

    "Umesema hali yake ni mbaya, una maana hatapona?"

    "Miriamu hakufafanu. Alichosema ni kwamba amefanyiwa operesheni ya hali ya juu ambayo hajapata kuiona."

    Kembo akapuliza moshi. Akasema "Chiko, Dk. Makete ni adui yetu mkubwa. Akipona, tumekwisha. Lazima tuhakikishe haponi."

    "Hiyo ni kazi ndogo kama kutafuna biskuti." Alisema Chiko. "Hata Hoza anaweza kuifanya."

    "Anacho kibweka?"

    "Kipo." Alijibu Hoza mwenyewe. Akainama na kuchomoa bastola kwenye soksi ya mguu wa kulia. Akaiweka mezani.





    "Ina sailensa?" Hoza akatikisa kichwa. "Haina."

    "Nitakupatia moja yenye sailensa." Kembo akatoa pochi nene na kulifungua. Akatoa kitita na kumkabidhi Chiko, akasema. "Utajua jinsi ya kugawa." Akamtazama kijana mdogo . "Hoza ukitenda kazi tuliyozungumza nitakupa milioni."

    "Fanya milioni mbili, mzee." Akasema Hoza. "Si kazi ndogo kama anavyodhani Chiko."

    "Ok. Lini?"

    "Hata leo usiku."

    "Good."





    *******************************





    Wazalendo Hoteli ilikuwa ghorofa moja, lakini ilichukua eneo kubwa. Ilikuwa Hoteli ya heshima. Harold Chisimba aliwakarisha wageni wake kwenye chumba alichokifanya sebule na ofisi yake, kilichopakana na chumba chake cha kulala.

    "Mimi ni Luteni Dennis Makete, na huyu ni Kachero Inspekta Bessy. Tumeelekezwa kwako na Kamishna Msaidizi...."

    "Nafahamu." Akamkatiza Chisimba. "Malik amenipigia simu na kuniarifu. Ameniambia niwape msaada wowote niwezao kuwapa kuhusu Kassim Hashir."

    "Tushukuru sana Bwana Chisimba." Alisema Bessy.

    "Sawa. Je niwapatie kiburudisho gani?"





    Denny akasema haraka. "Hapana, hapana Bwana Chisimba. Asante sana."

    Chisimba akainua mikono, kumaanisha 'mpendavyo.' Akasema, "Ni nini hasa mnachotaka kufahamu? Simuni Malik hakufafanua. Amesema mnaamini Kassim angali hai, na kwamba kuna mtu amemgonga na gari na kukimbia."

    "Amemgonga babangu, Dk,Raymond Makete, leo asubuhi. Tunaamini amemgonga kusudi."

    "Dk.Makete?" Chisimba akafinya uso kuwaza. Akasema, "Oh, ndiyo! Namkumbuka. Imekuwaje?"

    "Hatujui chochote." Alijibu Bessy, "Mzee Makete aliondoka nyumbani kwake akiwa mzima kabisa. Aliaga anakwenda benki kuchukua pesa. Pesa asichukue. Kassim alimgonga wakati anatokea benki. Tena kamgonga kusudi."





    "Mna hakika ni yeye aliemgonga."

    "Mzee Makete mwenyewe alisema, alipozinduka kwa nukta chache."

    "Ajali iliyomwua Kassim ilipotangazwa, niliwaambia watu kuwa ajali hiyo ni bandia, lakini wengi waliniona mpuuzi."

    "Kwa hiyo uko pamoja nasi?" Dennis aliuliza. "Yaani katika kuamini Kassim angali hai?"

    "Kabisa. Sikiliza. Laiti mimi ningekuwa ndiye Kassim ningefanya kama alivyofanya Kassim. Ningebuni ajali ya bandia."

    Dennis na Bessy wakakubali kwa vichwa. "Lakini kwa nini atake kumwua babaangu?" Dennis aliuliza.



    "Sijui." Alisema Chisimba, akajiwashia sigara, baada ya wageni wake kukataa karibisho lake la kuvuta. Kisha akasma ghafla, "Oh,subiri! Haiwezi kuwa kwa ajili ya lile tukio?"

    "Tukio gani?" Denny na Bessy waliuliza kwa pamoja.

    "Zaidi ya miaka ishirini na tano iliyopita, wakati wa utawala wa Mbelwa, Dk. Makete aliamini Kassim alimwua babake. Lakini hakuweza kufanya lolote kwa sababu Kassim na Mbelwa walikuwa marafiki. Akanieleza mimi, akidhani kuwa ningeweza kufanya lolote, kwa vile ni mwandishi. Nilipojaribu kufuatilia nikawekwa ndani."http://pseudepigraphas.blogspot.com/





    Bessy aliwaza kidogo kisha akatikisa kichwa. "Hiyo haiwezi kuwa sababu ya kutaka kumwua mtu, tena kwa gari. Kwa nini asijaribu mapema? Hata hivyo nitalifuatilia tukio hilo. Ni nani wa kunisaidia ?"





    "Dk. Makete mwenyewe." Alijibu Chisimba. "Au mkewe. Kwani yeye alikuwa nesi hapo hospitali wakati huo."











    Pombe ikampalia Kikoti. Radio ilikuwa inasema, "Dk. Makete aligongwa kusudi nyuma ya Benki ya Wakulima. Gari lililomgonga ni Benzi jeupe, likiendeshwa na mtu alievaa koti au jaketi la kunguru. Zawadi ya milioni moja iliyochangwa na wafanyakazi wa hospitali itatolewa kwa yoyote atakaesababisha mtu huyo kukamatwa."





    Kikoti akaanza kutetemeka. Kila kitu kilikuwa waziwazi. Yule bwana kulitazama gari lake upande wa mbele, kumuonyesha Isidori,kumpa koti lake la kunguru .....kila kitu.

    Hata yale maneno aliyoyadaka - 'ajali ...faini..heshima.' yalidhibitisha kitu kimoja tu. Tajiri yake ndie aliyetaka kumwua Dk. Makete. Sasa afanyeje? Alijiuliza. Lazima apate ushauri. Akawatazama wenzake. Akasema, "Bob! Butu! Mmesikia ajali iliyotangazwa?"





    "Ndiyo." Alijibu Bobu.

    "Inasemekana Dk. Makete amegongwa kusudi."

    "Mmesikia zawadi iliyotangazwa?"

    "Ndiyo."

    "Namfahamu aliemgonga Dk. Makete."

    "Unaleta masihara?"

    "Hapana. Ni kweli."

    Butu akauliza kidharau. "Sasa unataka tukusaidie kuibeba hiyo milioni?"





    "Kikoti!" Alisema Bob kwa sauti yake ya kisajini, "Unasema kweli au umelewa? Maana wisk hii si......"

    "Naapa. Nasema kweli. Mtu huyo ndiye tajiri yangu. Ana Benzi jeupe. Alirudi nyumbani boneti na bampa vikiwa vimeharibika. Alivaa koti la kunguru. Akaligawa haraka sana."



    Bob na Butu wakatazamana. Kisha Butu akamwambia Kikoti, "Unataka tukusaidie kuipata hiyo milioni? Utatumegea?

    "Ndiyo."

    "Subirini." Bob akainua mkono. Si ulisema tajiri yako ni kizito?"

    "Ni kizito kwelikweli."

    "Basi hii nafasi ambayo mtu hawezi kuipata mara mbili katika maisha yake."

    "Bob, unazungumza nini?" Butu aliuliza.

    "Huyo Makete anatuhusu nini sisi?"

    "Bob, mbona sikuelewi!"





    "Hii ni nafasi ya kuokota mamilioni, na sio kimilioni kimoja, tena cha kugawana watu watatu." Butu akatikisa kichwa. Akasema, "Naona unakuja na mawazo ya hatari Bob."

    "Hatari gani. Toka lini kuukacha umaskini, ulofa, ikawa hatari? Eti Kikoti, huyo tajiri yako hawezi kutupa milioni tatu ili tufumbe mdomo?"

    "Anaweza kutoa hata zaidi."

    "Unaona?" Bob aliumuuliza Butu.

    "Hapana, Bob, mimi simo.Tumefanya mengi ya kipuuzi, lakini hili litakuwa la kichizi." "Butu, utakuja juta. Utakufa bila kushika milioni mkononi mwako."

    "Potelea mbali."

    "Lakini....lakini...utatufichia siri yetu?"

    "Sina ninachokijua. Na hivi naondoka. Nakuacheni mwendelee na mipango yenu."





    *************************************





    "Mama, Kassim Hashir ndiye nani?"

    Walikuwa katika chumba cha mgonjwa. Bi mkubwa aliketi kwenye sofa, Bessy na Denny vitini. Bi mkubwa akashusha pumzi. Akasema "Denny, pengine babako amekosea."

    "Umeshamwona akisema neno au akitenda jambo bila ya kuwa na uhakika nalo?"

    "Basi tusubiri apate fahamu atakueleza mwenyewe ni nani huyo Kassim Hashir - iwapo ataamua kukueleza."





    "Mama, hatuna muda. Huyo hayawani anaweza kuihama tena nchi na kutoweka."

    "Yaani umeshapata habari zake!"

    "Ndiyo, za kijuujuu. Polisi wana faili lake, na mwandishi mmoja aliwekwa kizuizini kwa kufuatilia kifo cha babake. Inasemekana alimwua. Huyo mwandishi amesema wewe na baba mnakijua kisa hicho. Ni kweli?"

    Mama Denny akasita.

    "Mama, ni kweli au si kweli?"

    "Ni kweli."

    "Ndicho kilichomfanya atake kumwua baba?"





    "Sikioni kinahusika vipi." Bessy akaingilia, "Tueleze kisa hicho. Sisi tutaamua kama kina uhusiano na tukio la leo."

    Baada ya kusita tena, mama Denny akawasimulia kisa hicho......





    Wakati huo, zaidi ya robo karne iliyopita, hospitali hiyo ilikuwa ndogo tu. Dk. Makete na mama Denny walikuwa ndio kwanza waoane.

    Siku hiyo kama kawaida yao, walikuwa sehemu ya wagonjwa wapya,machela ilipoletwa, ikifuatiwa na msichana wa miaka kumi na mbili, aliyekuwa analia. Wakati mama Denny anamfariji msichana huyo, Dk. Makete alilifunua blanketi akaitazama maiti. Ilikuwa ya mzee wa kati ya miaka hamsini na sitini. Shingo yake ilikuwa imevunjika.





    Akaifunika tena na kusema, "Hakuna cha kufanya. Amesha kufa. Amevunjika shingo. Apelekwe chumba cha maiti."

    Mama Denny akasema, Rey, unamfahamu marehemu?"

    "Hapana. Ni nani?"

    "Othman Hashir."

    Dk. Makete akaifunua tena maiti na kuitizama sura. Akasema, "Oh, my God! Ndiye. Imekuwaje?"





    Msichana akasema huku akiendelea kulia, "Amesukuma."

    "Ni nani aliyemsukuma?"

    "Kaka Kassim, alimsukuma ghorofani, akabiringika kwenye ngazi."

    "My God! Lazima turipoti polisi."

    Dk. Makete alipofika Kituo cha Kati, akawekwa benchi asuburi karibu saa nzima. Hatimaye akapelekwa kwenye ofisi ya afisa mmoja wa cheo cha juu.





    "Ndiyo, Dk. Makete?" Hakuambiwa aketi. Akasema, "Nimekuja kutoa taarifa ya kifo cha Mzee Othman Hashir. Binti yake anasema kaka yake Kassim Hashir alimsukuma kusudi kwenye ngazi. Kifo kimesababishwa na kuvunjika shingo."



    "Dk. Makete," Alisema afisa huyo wa polisi, "Unataka kuyatia maanani maneno ya mtoto mdogo? Nimeambiwa hafiki hata miaka minane."

    "Ana zaidi ya miaka kumi."

    "Oh, sawa. Tutafanya uchunguzi. Ila ningekushauri uzingatie zaidi kazi yako kuliko kujihusisha na mambo mengine, mambo yasiyokuhusu."

    "Ni wajibu wangu kuripoti mauaji." Dk. Makete alisema.

    "Sawa. Umesharipoti. Ni juu yetu kuamua kama ilikuwa ajali au mauaji kama unavyodai. Kwisha."









    "Usiwe na wasiwasi." Kembo alimwambia Kassim. "Nimepata kijana jasiri wa kuifanya ile kazi. Ataifanya usiku huu. Ametaka milioni saba."

    "Sawa."

    Wakikuwa sebuleni, wakinywa mvinyo kabla ya chakula cha jioni. Simu ikaita. Kembo akaenda kuisikiliza.

    "Hallo."

    "Bwana Kessy?" Ilikuwa sauti nzito.

    "Hapana."http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    "Nataka kuzungumza naye."

    "Nimwambie nani anayetaka kuzungumza naye?"

    "Bob."





    Kembo akauziba mdomo wa simu na kusema, "Mtu aitwaye Bob anataka kuzungumza nawe." Kassim akainua nyusi. "Bob nani?"

    Kembo akasema simuni, "Bob nani?"

    "Bob tu inatosha. Mwambie ni mhimu sana aje simuni. Ni kwa manufaa yake."

    Kembo akamwambia Kassim, "Anasema Bob tu inatosha. Anasema ni mhimu sana."





    Kassim akainuka na kuupokea mkono wa simu. Akasema, "Yes?"

    "Bwana Kessy?"

    "We ni nani? Kwa kawaida sizungumzi na watu nisiowajua."

    "Hiyo ni kawaida mbovu. Ungekula hasara kubwa kweli kweli."

    "Una maana gani?"

    ""Hukuisikiliza taarifa ya habari?"

    Akibana pumzi, Kassim akauliza, "Inanihusu nini?"





    "Looh! Inakuhusu sana. Tena sana. Unajua, kuna daktari mmoja aliyegongwa na gari leo asubuhi, nyuma ya Benk ya Wakulima. Wameitangaza habari hiyo. Wamesema kuna zawadi milioni...."

    "Unataka kiasi gani?"

    "Saba tu Bwana Kessy."

    "Laki saba?"

    "Laki saba ni kitu gani siku hizi ndugu yangu? Hata banda la kuku hujengi. Nazungumzia milioni saba."

    "Unazitaka lini?" Kassim akauliza kwa sauti kavu.

    "Biashara sampuli hii bwana Kessy huwa hailazwi,"





    "Hujui habari kuwa benki hufungwa usiku? Au unadhani naweka nyumbani kiasi kikubwa kama hicho? Ni wapumbavu tu wafanyavyo hivyo."

    "Ah, we ni mtu mkubwa bwana Kessy. Huwezi kukosa ndugu, jamaa na marafiki wa kukuazima kiasi kidogo kama hicho."

    "Milioni saba ni kiasi kidogo?"

    "Oh, kwa mtu kama mimi ni hela nyingi sana. Lakini kwa mtu kama wewe......"

    "Nipigie simu baada ya masaa mawili."

    "Maneno si hayo bwana!"





    Kassim akaurudisha mkono wa simu kwa nguvu. "Vipi?" Kembo aliuliza.

    "Balaa jingine. Anafahamu. Ni Mungu ajuaye ni nani mtu huyo na amejuaje. Anataka milioni saba."

    "Nazo ndiyo huna hapa nyumbani?"

    "Nina zaidi ya milioni ishirini ndani ya sefu." Kassim alifoka. Akajizatiti na kuzungumza kwa sauti ya kawaida, "Nimetaka muda wa kufikiri."

    "Pana cha kufikiri? Nilikwambia kitendo ulichotenda ni cha kipumbavu sana."





    "Mbona unanitia wasiwasi Kembo?"

    "Nakutia wasi wasi?"

    "Ndiyo. Yaelekea unapendelea nililipe hilo baradhuli."

    "Sioni kama njia nyingine."

    "Unajuaje kama hatakuja kudai tena? Anaweza kunigema hadi shilingi yangu ya mwisho." Kembo akabaki mdomo wazi.





    "Kinachonitia wasiwasi zaidi ni kule kufichuka siri hii. Ninavyoamini, mnaifahamu watu wawili tu. Wewe na Isidori."

    "Bwana Kessy," Kembo akasema kwa mshangao,"Unataka kunitilia mashaka mimi!"

    "Kwa vyovyote msaliti hawezi kuwa Isidori. Kwanza, kama unavyofahamu, tuko nae hapa hapa nyumbani. Hajatoka na hana mawasiliano yoyote ya simu. Pili, ananihusudu vibaya vibaya sana. Yuko tayari kufa kwa ajili yangu."





    Kembo akatikisa kichwa akasema, "Nitakwamia jambo moja. Ili kukutoa kabisa mashaka , mimi mwenyewe nitamkomoa mtu huyo na kukuonyesha maiti yake."





    **************************************





    "Mama, hiyo inaweza kuwa ndio sababu ya kumfanya Kassim atake Kumwua baba?"

    "Mlisema nikikuelezeni, mtaamua wenyewe."

    Denny akamtazama Bessy, ambaye alitikisa kichwa. Denny akamwuliza mamake. "Kwa nini baba aliendelea kumfuata fuata Kassim?"

    "Hakuendelea." Alijibu Bi mkubwa. "Alichofanya ni kumfahamisha Harold, huyo mwandishi."





    Denny naye akatikisa kichwa. Akasema, "Mama, kuna kisa kingine." Mama Denny akabaki kimya. "Mama, nakuomba utueleze."

    Badala ya kujibu, Bi mkubwa huyoo akadondosha tone la chozi.

    "Oh, Mungu wangu!" Dwnny akainuka haraka na kupiga magoti mbele ya mamake. Akaufumbata mkono wake. "Niwie radhi mama."





    Bessy akasema, "Denny, umefika wakati wa kumpeleka nyumbani mama."

    "Utaweza kuilinda ngome peke yako?" Denny alimwuliza Bessy akimtazama kwa macho makali.

    "Kama unadhani nimepewa Uinspekta kwa sababu ya sura yangu, umekosea."

    "Twende nikupeleke nyumbani mama."





    Bi mkubwa akainuka kwa kujizoazoa polepole akisaidiwa na Denny. "Sitakawia kurudi." Alimwambia Bessy.

    "Oh, usiwe na wasi wasi. Kula, oga, badili. Utanikuta hapahapa." Bessy alisema akiokota gazeti.

    Denny akaufungua mlango na kumtanguliza mamake. Ukumbini akamshika mkono na kumwongoza kwa hatua za kizee.





    Ngazini, wakiteremuka kwa hadhari, wakapishana na kijana anayepanda kwa hima. Denny hakumtazama mara mbili. Hadi walipokuwa kwenye ngazi za ghorofa ya kwanza ndipo kengele ya hatari ilipogonga kichwani mwa Dennis.

    "Mama!" Dennis akauachia mkono wa mamake. "Yule kijana haonyeshi kuwa daktari! Nisubiri hapa hapa!"





    Akaanza kuzipanda ngazi mbili mbili.

    Macho yake kwenye gazeti, masikio yake yakanasa kitu kama hatua zilizokoma ghafla. Bessy akainua kichwa na kuutazama mlango.Kitasa kilikuwa kinazunguka pole pole.





    Kufumba na kufumbua, Bessy akawa nyuma ya sofa, mgongo wa kiti hicho umemziba kabisa, ameshaufungua mkoba wake, ameshaitoa bastola, iko imara mkononi, tayari imeshakokiwa.

    Akachungulia kwa chini ya mgongo wa sofa, siyo kwa juu. Akauona mlango ukifunguliwa taratibu.





    Cha kwanza kupenya ndani kilikuwa ni sailensa. Kisha bastola yenyewe na mkono. Na mwisho nusu ya kiwiliwili cha mtu.

    Alikuwa Hoza. Akayazungusha haraka macho yake mekundu humo ndani. Akaamini hamkuwa na mtu mwingine humo ndani zaidi ya mgonjwa aliyelala kitandani.

    Hayo yote yalitendeka katika nusu nukta.

    Bessy akimwona Hoza wazi wazi, akaamuru. "Dondosha chini bastola yako. " Sauti yake ikavuma humo ndani.





    Hoza akashtuka. Akayaondosha macho yake kitandani na kuyazungusha tena humo ndani. Asione mtu.

    Akamlenga Dk. Makete .

    Bessy akabana pumzi na kukivuta kilimi cha bastola yake. Ikalipuka kwa kishindo cha kumtia mtu uziwi wa muda.

    Risasi akakita katikati ya paji la uso na kuwa kama ndonya ya Kigogo. Nguvu zake zilimsomba Hoza, zikamrusha kinyumenyume, na kumbwaga kwenye korido, kando ya miguu ya Dennis aliyewasili nukta hiyo hiyo.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/



    Dennis akautazama mwili wa Hoza na kuiona ndonya. Akauliza kwa ukali, "Ilikuwa lazima?" Bessy akiwa ameshainuka, na yuko katikati ya chumba, akafoka, "Una maana gani 'ilikuwa lazima'?"

    "Ilikuwa lazima umwue? Angekuwa hai tungemhoji."

    "Na mzee angekuwa amekufa." Bessy alijibu.

    "Au unataka kuniambia hiyo bastola yake ni ya bandia?"





    Dennis akaitupia jicho bastola yenye sailensa iliyokuwa kwenye korido,hatua kadhaa mbali na maiti. Haikuonyesha mzaha hata chembe.

    Denny akainua mikono na kusema, "Yamekwisha."

    "Bora yaishe." Akasema Bessy kwa sauti yake tulivu ya kawaida. "Watu wanaanza kusogea sogea."

    "Ilete ndani bastola yake." Dennis alimwambia, akiinama na kuishika miguu ya maiti.

    Bessy akaguna, "Denny!"

    "Kitu gani?"

    "Hatupaswi kitu chochote. Inapasa kupiga simu kituoni na kuwaarifu wenzangu. Watakuja...."

    "Achana nao. Utawaarifu baadaye. Ilete bastola yake." Dennis akasema akiiburutia maiti chumbani.





    Bessy alisita kidogo, kisha akabetua mabega na kuokota bastola ya Hoza. "Iweke mezani." Dennis akamwambia. "Nenda kwenye ngazi za ghorofa ya kwanza, mchukue mama umtafutie usafiri."









    Bessy akakubali kwa kichwa na kutoka . Denny alipokuwa anaufunga mlango, mwuguzi msimamizi wa wodi hiyo akataka kuingia. Denny akamzuia.

    "Pametokea nini?" Aliuliza mwuguzi huyo, akijaribu kuchungulia ndani, macho yamemtoka pima.

    "Tatizo dogo tu." Denny akamjibu. "Kaendelee na shughuli zako."

    "Nimesikia mshindo. Kama .... kama bunduki."

    "Ilikuwa ni bastola ya Inspekta Bessy. Usiwe na wasi wasi . Taarifa kamili utaipata baada ya muda mfupi tu.





    Mwuguzi akasita, akiona vigumu kuondoka bila ya kuingia ndani na kuchunguza kama wajibu wake ulivyo. Lakini hapakuwa na nafasi ya kupenya ndani bila kutiana mieleka na kijana huyu. Na hilo halikuwa katika ajenda yake ya wakati huo.

    Hatimeye akauliza. "Mzee Makete yupo salama?"

    "Kama hazina ya taifa." Dennis akamhakikishia. "Usiwe na wasiwasi hata chembe. Nakuzuia kwa sababu kuna kazi ndogo ya kipolisi. Inspekta Bessy ameua jambazi lililoingia na bastola. Lakini hakuna madhara yoyote kwa babangu."



    Mwuguzi akaonyesha kuridhika. Dennis akaufunga mlango. Akaichukua bastola yenye sailensa na kuichunguza. Akashangaa wapi watu hawa wanapata silaha za hatari kama hiyo!

    Akairudisha bastola mezani na kuigeukia maiti. Baada ya kuitizama kwa nukta moja au mbili akaanza kushughulika.





    Aliivua nguo zote, hata chupi. Kisha akazipekua kwa uangalifu, akitoa kitu kimoja kimoja, akakiangalia kwa makini kabla ya kukiweka mezani.

    Bessy aliporejea, alikuta akiigeuza maiti na kuichunguza. Mwana mama akalalama. "Mtume! Dennis unafanya nini? Hiyo si kazi yetu! Kuna watalaamu...."





    "Ambao huchukua siku kadhaa kuichunguza maiti, wakiringia utalaamu wao, kisha wakueleze jambo ambalo ungefahamu katika dakika mbili tu!"

    Bessy akashusha pumzi na kujibwaga kwenye sofa. "Denny, wakuu wangu wakigundua nimekuacha ufanye hivyo...."

    "Hukuniacha. Hukuwepo. Ulikwenda kumtafutia mama usafiri. Je, umempatia?"

    "Ndiyo. Nimemchukulia teksi."

    "Hakukudadisi?"

    "Alitaka kujua ule mshindo ulikuwa wa nini."

    "Ukamwambiaje?"

    "Tanki la maji limepasuka."





    Dennis akakubali kwa kichwa, akiwa ameridhika. Akasema. "Sawa kabisa."

    Bessy akauliza, "Denny, kitu gani kilichokurudisha? Yaani ulipotoka na mama?"

    "Huyu nyani. Nilipishana naye ngazini. Lakini sikumtanabahi hadi nilipokuwa kwenye ngazi za ghorofa ya kwanza."

    "Kitu gani kilichokufanya umshuku?"

    "Macho yake na nywele zake." Dennis alijibu, akiendelea kuikagua maiti.

    Bessy akasema, "Denny kadri ninavyochelewa kupiga simu kituoni, ndivyo unavyozidi kunitia matatani."



    "Nipe dakika mbili au tatu tu zingine."











    Watu wanne waliketi wakinywa na wakisubiri kwenye sebule ya nyumba Namba 21 mtaa wa kitosi, eneo la Buffalo Hill. Kessy au Kassim Hashir na Kembo waliketi upande mmoja wakinywa kimya, nyuso kavu. Chiko na Fensy waliketi upande mwingine wakinywa huku wakizungumza na kucheka.





    Baada ya muda Kassim akaitazama saa yake ya dhahabu na kusema. "Kwa nini huyu mwanaharamu hapigi simu? Tulikubaliana masaa mawili, yanakaribia masaa matatu sasa!!"

    "Anataka uvuje jasho kidogo." Kembo alimwambia. "Anataka utaharuki. Katika hali hiyo unakuwa fal@ zaidi, unafanya chochote anachosema, tena mbio mbio."

    "Mwana wa mbwa koko."





    "Sikiliza Bwana Kessy, atakapopiga simu ni mimi nitakayezungumza naye, siyo wewe. Na nyote pamoja na nyinyi Chiko na Fensy - mtanyamaza kimya kabisa. Akijua tuko wengi anaweza kugutuka. Tumeelewana?"

    "Ndiyo."

    "Nitajaribu kuiga sauti yako."

    Kembo aliendelea akimtazama Kassim.





    "Pengine ni mtu anayekufahamu."

    "Sidhani." Akasema Kassim. "Sauti yake ilikuwa ngeni kabisa."

    "Anaweza kuwa ameibadili, simuni kitu kama hicho ni rahisi sana." Kengele ya simu ikalia. Akasema. "Hapana hata kukohoa kwa sauti."

    Kila mmoja akakubali kwa kichwa, kama vile kipindi cha ukimya kimeshaingia.





    Kembo akainuka akaenda kwenye simu, akauinua mkono wa kusikilizia na kuuweka sikioni. Akiigiza sauti nzito ya Kassim akasema, "Yes?"

    "Bob."

    Kikapita kimya cha nukta mbili au tatu kisha. "Je, mwenzangu ni Bwana Kessy?"

    "Ndiyo."

    Kimya kingine kifupi kisha, "Je, umefanikiwa?"

    "Ndiyo." Kembo alijibu.

    "Zote saba?"

    "Ndiyo."





    "Very good. Sasa sikiliza kwa makini. Saa sita kamili uendeshe gari lako kwenye barabara ya Kaskazini. Ukilivuka tu daraja la Singisa utaona kibanda cha simu mkono wa kushoto."

    "Nakifahamu."

    "Good. Ufikapo hapo punguza mwendo, rusha mkoba wenye fedha na uendelee na safari yako.

    "Umenipata?"

    "Vizuri kabisa."

    "Very good. Usiku mwema."

    "Subiri." Kembo akasema haraka.

    "Nini tena?"

    "Najuaje hii itakuwa ndiyo alfa na omega?"

    "Una maana gani?"

    "Najuaje hurudi tena kutaka fedha zingine?"





    "Bwana Kessy mimi si fisi. Hivyo sina tamaa ya fisi."

    "Kudai milioni saba siyo tamaa ya fisi?"

    "Unataka nikachukue milioni iliyotangazwa? Sikiliza we fal@. Mimi nakufanyia hisani kubwa sana. Dk.Makete yu mahututi. Ulimgonga kusudi. Lilikuwa jaribio la kuua. Hata akipona, unaweza kufungwa maisha."





    Kikapita kimya cha zaidi ya nukta kumi, kila pande ikipumua kwa nguvu. Hatimaye Bob akauliza.

    "Umenipata vizuri?"

    Kembo akasema, "Wewe ni mwanaharamu, mtoto wa mbwa koko, mjaa mavi uliyelaaniwa."

    "Umemaliza?"

    Kembo hakujibu

    "Bob akaendelea. "Itasaidia nini? Hata ukinitwisha kontena zima la matusi, itasaidia nini? Wewe umeshaimeza ndoano na mshipi wake. Hufurukuti. Utafanya uambiwacho."

    "Usiwe mpumbavu kiasi hicho. Mimi nina pesa. Naweza kuyeyuka sasa hivi."





    Bob akapumua kwa nguvu, kama aliyepigwa ngumi ya tumbo. Pumzi zilipomrudia akasema, "Polisi watakusaka. Watajua ni wewe uliyemgonga Makete. Habari zitazagaa magazetini. Heshima yako kwisha. Pamoja na mamilioni yako, utaishi kama panya ndani ya shimo."

    Kimya cha safari hii kilichukua karibu dakika nzima.





    Hatimye Bob akasema, "Sema fyoko!"

    Kembo hakusema

    Bob akaunguruma kwa sauti yake ya kisajenti. "Saa sita kamili."

    Simu ikafa. Taratibu Kembo akaurudisha chini mkono wa simu.





    Kassim akasema, "Kembo, palikuwa na haja ya kubishana naye vile?"

    "Alinijazibisha, mwana hizaya." Alijibu Kembo. "Mambo yakienda kombo ataleta ushenzi." Alisema akiwakazia macho Chiko na Fensy na kuongeza, "Kwa sababu hiyo sitaki yaende kombo. Mmesikia, sitaki mboronge."





    "Amesema saa sita kamili." Kembo akasema akirudi mahali pake. Akaitazama saa yake. "Tuna muda wa kutosha."

    Akajitilia kinywaji, akakimeza na kuendelea.

    "Pesa zikadondoshwe kwenye kibanda cha simu cha karibu na daraja la Singisa saa sita kamili. Amejua kuchagua mahali pazuri, kwake na kwetu. Mahali hapo saa sita kamili ni sawa na makaburini.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/



    Akajiwashia sigara na kuendelea, akiwaambia Chiko na Fensy. "Mahali hapo pana sehemu nyigi za kujibana, mojawapo ikiwa ni chini ya hilo daraja."

    "Tunapafahamu." Alisema Fensy.

    "Kumsubiri huyo Bob. Lakini msifanye lolote mpaka mmwone akiuufuata mkoba wa fedha na akiinama kuuchukua. Msije mkamdhuru mtu mwingine, ingawa uwezekano huo ni mdogo sana kwa mahali hapo saa hizo. Sawa?"

    "Sawa." Vijana hao walijibu wakimalizia vinywaji vyao.





    "Itakuwa ni vizuri zaidi kama mtamshika akiwa angali hai, ili tumhoji kwanza. Tujue siri hii ameijuaje, na kama kuna mtu mwingine anaijua."

    "Sawa. Tunajua nini cha kufanya." Alisema Chiko.

    "Mimi nitakuja na fedha saa sita kamili. Nitaudondosha mkoba na kuendelea na safari kama alivyoagiza."

    "Sawa."





    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog