Search This Blog

Sunday 20 November 2022

NJIA NYEMBAMBA - 3

 





    Simulizi : Njia Nyembamba

    Sehemu Ya Tatu (3)





    “Usihofu, ni jambo dogo tu hilo.”

    “Nashukuru sana. Nimewakumbuka sana wazazi wangu, nataka tukienda Sierra nikawasalimie.”

    “Tutaenda wote, natamani nikusindikize.”

    “Nitafurahi mno.”

    Baada ya hiyo kauli ghafla sauti ya kengele ikasikika kwanguvu, Amadu akashtuka.

    “Kengele ya nini hiyo?”

    “Sijui!” Chui alijibu huku naye akiwa na kauso kenye kabumbuwazi. Amadu alitizama saa yake ya mkononi akatikisa kichwa chake na kutabasamu kama vile ameona kitu cha kijinga.

    “Ni wakati wa kula kumbe!”

    Chui naye akatabasamu. Walinyanyuka wakaenda kupata msosi. Watu walikuwa wanmashangaa Chui, alikuwa ni mpya miongoni mwao. Wengine walishindwa kunyamaza wakamuuliza ni wapi alipotokea wakati wengine wakiyarushia hayo maswali kwa Amadu ambaye ndiye alionekana naye karibu.

    “Huyu ni mdogo wangu!” Amadu alimjibu mmoja wa wa mtu aliyemuuliza kisha akatizamana na Chui na kucheka. Walipomaliza kula, Amadu akabebelea chakula kiasi na kumpelekea Ulsher pamoja na mzee Buruwani.

    Asubuhi ya saa moja kamili ilipohitimu, kengele ya makutano ikagongwa. Wafuasi wote wakakutana kwenye uwanja wao, Kessy akatoka makao makuu na kwenda kukutana nao. Dhamira kuu ya mkutano ikawa moja tu, kumtambulisha Chui kama mfuasi wao mpya na apewe ushirikiano wote katika kila shughuli ya ukombozi. Lakini zaidi ya hapo, Amadu pamoja na Chui wakaitwa na Kessy waongozane naye kuelekea makao makuu, huko Kessy akawapa kazi mpya ya kufanya.

    “Nataka mkavamie shule hizi tatu za msingi. Mkawateke watoto wa kutosha muwalete hapa. Tunahitaji kuongeza ukubwa wa jeshi letu, tumepoteza wanaume wengi.”

    “Ila general, hakuna njia nyingine zaidi ya hiyo?” Amadu alitia kaswali.

    “Hakuna njia nyingine. Au wewe una wazo?”

    “Ndio.”

    “Niambie.”

    “Mi nadhani tutumie tu njia zile zile tunazozitumiaga kuliko kuumiza hao watoto na kuwatenganisha na wazazi wao.”

    “Hapana! Hakuna tena pesa ya kutosha kufanya hivyo. Pesa iliyobakia inatosha tu kuleta madawa ya kulevya kwaajili ya kuwazubaisha na kuwaingiza hao watoto kwenye mfumo. Hatuwezi tena kuwashawishi watu wazima. Kuwapata watoto ni rahisi, pia wanakuwa watii zaidi pale wanapopewa mafunzo ya kutosha kuliko watu wazima.”

    “Ila general …”

    “Sitaki tena maswali wala mawazo. Fanya nilichokuambia. Inabidi ujifunze kutii amri zaidi ya kupinga amri. Mnaweza mkaenda kwa sasa, kesho muda wa mchana mtakwenda huko Sierra kutimiza agizo.”

    Kikao kikafungwa na hiyo amri. Amadu pamoja na Chui wakatoka makaoni na kwenda kujumuika na wenzao kwenye mazoezi. Walibeba vitu kupasha misuli. Walikimbia kwenye vilima kutafuta nguvu za miguu na stamina. Walifanya mazoezi ya kulenga shabaha kwa risasi wakifanya shindano miongoni mwao. Zoezi lilipokoma, Amadu pamoja na Chui wakaelekea mtoni kuoga. Na huko ndipo Chui akamuona Amadu hayupo sawa. Hakuwa na tabasamu lake lililozoeleka. Uso wake ni wazi ulimezwa na tafakuri fulani.

    “Amadu, nini kinatafuna akili yako?” Chui aliuliza. Amadu akazamia ndani ya maji kwa muda wa dakika kama mbili kisha akainuka. Akamkuta Chui bado amesimama kama mtu amngojeaye mgeni akitokea safarini.

    “Siko tayari kwenda kuteka wanafunzi.”

    “Kwanini?”

    “Sijaona haja ya kuja kuwatesa watoto huku. Wanahitaji kusoma, wanahitaji kukaa na wazazi wao. Kuwateka na kuwaleta huku ni sawa na kuwafanya wateseke. Si lengo letu ama langu kuwatesa wana Sierra wenzangu, bali kuwakomboa.”

    Chui alitikisa kichwa chake kama mtu asikitikaye kisha kamuangalia Amadu.

    “Hamna njia kaka. Sasa utafanyaje? … Cha kufanya ni kuwachukua hao watoto na kuwaleta hapa kwa amani. Wapatiwe mafunzo, baadae watakuja elewa.”

    “Si rahisi kihivyo, Chui. Si watoto wote watakaoweza kustahimili. Wengine watakufa mazoezini wakati wengine wakiharibikiwa moja kwa moja na utumizi wa madawa, hata msongo wa mawazo.”

    “Naelewa sana hiko unachokiongea. Ila general amebakiwa bila jinsi na hiyo ndio ameona njia pekee. Nadhani itabidi tufanye tu.”

    Amadu hakusema tena jambo. Alizamia chini ya maji akakaa kwa muda wa dakika moja, alipoibuka alikuwa na tabasamu. Alimshika mkono Chui akamuambia;

    “Tushindane kuzamia.”

    Baada ya hilo neno, wakaanza kushindana nani akaaye muda mrefu kwenye maji kwa kuhesabiana muda. Amadu akashinda hilo zoezi kwa mara tatu akimuacha Chui kwa nyuma mno.

    “Hatimaye na wewe umekaa nyuma. Si ulinishinda kwenye kulenga shabaha!”

    Amadu alisema kwa bashasha la furaha wakaanza kumwagiana maji. tendo hilo likadumu kwa muda wa dakika zisizozidi dakika kumi. Wakatoka kwenye maji na kurudi kambini, wakati huo jua laenda kuzama ila bado miale yake inasema na uso wa dunia.

    Wakiwa wanatembea kuelekea hemani, kwa mbali Amadu na Chui wakaona wafuasi wenzao wanajenga nyumba za miti. Walizitizama, Chui akauliza;

    “Wanajenga nini?”

    “Nyumba za hao watoto tutakao kwenda kuwakamata.” Amadu alijibu kwa sauti ya chini. Kwa muda wakatizama zoezi lile likifanyika, giza lilipoanza kudhoofisha uwezo wa macho yao, wakaondoka na kwenda hemani. Asubuhi ya mapema, wakaaamka na kuanza kujiandaa kwa zoezi lao lililo mbele. Walipakia bunduki kadhaa zisifike hata tano kwenye basi, lile walilowahi kuliteka Sierra hapo awali, wakabebelea na maji ya kunywa. Wakawasha basi tayari kwa kuhepa. Wakati wanatoka, general akawasimamisha kwa kusimama mbele yao.

    “Nataka muende na hawa.”

    General alinyooshea mkono wake mlangoni mwa makao makuu. Wakatoka Talib na Mohamed. Amadu akang’aka;

    “Hayakuwa makubaliano yetu general.”

    “Nilikuambia jana, jifunze kutii amri zaidi ya kupinga. Utaenda nao.”

    Amadu alitaka tena kufungua kinywa alonge ila Chui akamshika mkono na kumminya kama ishara anyamaze.

    “Ina mana hatuamini, au?” Amadu alimuuliza Chui kwa sauti ya kunong’oneza

    “We tulia tu, kaka. Tufanye tu.” Chui naye alinong’oneza. Talib na Mohamed wakapanda basi na kuanza safari.

    Kwa dakika kama kumi na tano wakiwa njiani hakuna aliyemuongelesha mwenzake. Safari ilikuwa ya kimya, kelele tu ya basi ikisikika. Lakini ilipohitimu dakika ya kumi na sita, Talib akavunja ukimya;

    “Tunaanza na shule gani?”http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Hakuna aliyemjibu. Kila mtu alikuwa na yake.

    “Nimeuliza, tunaanza na shule gani we Amadu. Hunisikii?”

    “Kwani mkuu hajakuambia?” Amadu alijibu kwa kuuliza.

    “Nimekuuliza wewe!”

    “Tulia, utaona.” Amadu alijibu kibabe. Chui akaingilia kati;

    “Tunaanza na shule ya Devout.”

    Talib akatabasamu kwa kebehi na kusema;

    “Kwahiyo wewe ni kibaraka wake, sio?”

    Chui akamtizama Talib bila ya kusema jambo. Akageukia mbele na safari ikajongea.

    “General ameniambia niwatizame kwa makini. Na nihakikishe kila kitu kinaenda sawa. Kama mnabisha muulizeni Mudy hapa.”

    Talib alijibaraguza. Bahati mbaya hakuna aliyehangaika naye tena, wote waliweka midomo yao kufuli. Walipokaribia eneo la shule wanayoivamia, Amadu akatoa maelekezo;

    “Shule ina madarasa matano na ofisi mbili. Hatuwezi tukajigawanya kutosha kote huko. Tutakachokifanya ni kuwatoa wanafunzi wote nje wakusanyike eneo moja. Talib na Mudy, nyie mtaenda ofisini na kuwaweka walimu na wafanyakazi wote chini ya ulinzi.”

    Baada tu ya hayo maelezo, basi la wakina Amadu likagonga geti la shule na kuingia ndani. Kabla hawajashuka, Amadu akatoa angalizo;

    “Hakuna kuua!”

    Walijigawanya kama vile walivyopena maelezo. Ndani ya dakika tano, wanafunzi wote wakawa wapo nje ya madarasa, mikono kichwani. Nyuso zao zikiwa zimetawazwa na hofu kubwa, wengine wakilia na hata kutiririsha makamasi. Amadu pamoja na Chui wakachagua wanafunzi wa kiume ishirini kwa kuwagusa na bunduki za na kuwataka wakajipakie kwenye gari. Waliwachagua wale wanafunzi walioonekana wameshiba na wana miili ya mapambano. Wakiwa katika hilo zoezi, ghafla wakasikia sauti ya milio miwili ya risasi toka ofisini mwa walimu. Amadu na Chui wakatahamaki kwa kutizamana. Upesi, Amadu akaelekea huko zilipotoka sauti za risasi, akakuta wanaume wawili chini wamelala damu zikiwa zikiwa zinawachuruza vichwani. Talib akiwa ndiye aliyeshikilia bunduki kama mtu aliyetoka kushambulia.

    “Si nilisema hakuna kuua?” Amadu alifoka.

    “Sasa kama analeta ubishi?” Talib alijibu na kuongezea, “najua ninachokifanya. Sihitaji kuelekezwa, sawa?”

    Kabla Amadu hajajibu, mluzi uliita huko nje akaamua atoke na kumrudia Chui wakamalizia zoezi lao la kuchagua watoto kisha wakaondoka toka eneo lile la shule. Wakaacha simanzi pana na hofu ndefu kwa wanafunzi na walimu.

    “Wamemchukua kakaaa!” Mwanafunzi mmoja mdogo mwenye makadirio ya umri wa miaka saba, alipaza sauti kwa kulia. Mwalimu alimbembeleza na kumtaka anyamaze. Lakini haikufua dafu, kwani wanafunzi wengine nao walianza kulia, na hata baadhi ya walimu ambao walishindwa kuvumilia kuona mizoga miwili ya wenzao imejilaza kinyama.

    Palikuwa eneo la msiba ghafula. Nyuso zao za tashtiti ya majonzi ziliwalilia waliouwawa na wale waliobebwa. Hata pale taarifa zilizopotolewa kituo cha polisi, haikuwa tena na faida kwani watuhumiwa walikuwa tayari wameshayeyuka ndani ya nchi ya Sierra, sasa wakiwa ndani ya Guinea.

    “Ndio mkuu … inasemekana wameelekea Guinea, sasa tunafanyaje?” Polisi mmoja akiwa na wenzake kama nane wakiwa na bunduki, aliongea na simu yake.

    “Ok … sawa, mkuu tunarudi.”

    Polisi alikata simu yake na kuwataka wenzake warudi kwenye gari wakayoyoma. Baada ya masaa matatu, kukawa na kikao ndani ya jengo la wizara ya ulinzi. Wanaume wanne na mwanamama mmoja wakiwa wamevalia nguo za kijeshi na polisi zikiwa zimechafuliwa na vyeo, waliketi wakikitizama kiti kimoja kilichokuwa tupu, ambacho baada ya muda kilikaliwa na mwanaume mmoja aliyevalia suti ya kaki baada ya kupewa salute na wengineo. Kikao kikafunguliwa.

    “Sasa hatuna tena haja ya kukaa na kungoja. Ni wazi kabisa tena isiyopingika kwamba washenzi hawa wana makazi yao nchini Guinea. Hatuwezi tukakaa kungoja mpaka turuhusiwe, si jambo la mashaka raisi wa Guinea anawafichama hawa watu.” Mwanaume pekee aliyevalia suti alitamka.

    “Ni kweli, mkuu. Ila kama tumeshindwa kupambana nao na kuwatoa mji wa Kabala, huko ndani ya Guinea tutaweza kweli?” Aliuliza mwanamama pekee kikaoni.

    “Hapana! Si kwamba tumeshindwa.” Alidakia mjumbe mwingine wa kikao. “Endapo kama tukienda na kuvamia moja kwa moja Kabala, tutawaua wananchi wetu wengi mno maana wapo hapo kama mateka. Inabidi tutumie busara zaidi kuliko nguvu.”

    “Kweli.” Mjumbe mwingine naye akadaka mada, “Tulikuwa tunaenda vyema sana kipindi kile tunapata msaada toka Liberia. Ila tokea na wao waanze kushambuliana na Le tueurs baada ya kuuweka mji wa Monrovia chini yao imekuwa tena vigumu. Ila kwa mimi, namuunga mkono mkuu. Tuna haja ya kwenda huko Guinea. Ila … Ila ni kwa siri kwa maana isipokuwa hivyo, tutakuwa tumetangaza vita na Guinea. Na hatutoweza kuwamudu pande zote mbili, waasi wa MDR na wanajeshi wa Guinea. Inabidi tuchague makomando kadhaa, wakapeleleze na hata kuteketeza kambi ya waasi huko.”

    “Naunga mkono hoja.” Mjumbe mwingine akadakia. “Waasi waliokuwepo Kabala, wanapata msaada toka kwa wenzao waliopo Guinea. Kama tukifanikiwa kuwamaliza wa huko Guinea, hawa wa Kabala watakuwa yatima, na tutawamaliza kwa urahisi mno.”

    Hoja hizo zikaonekana kukubalika. Ikadhamiriwa kupangwa kama ilivyotamkwa. Mkuu akaongezea kwa kuuliza;

    “Kuna lolote zaidi ya hayo?”

    Mwanamama pekee kikaoni akatoa picha tano na kuziweka juu ya meza. Mkuu akazichukua na kuzitizama.

    “Hawa si ndio wale wale uliowahi kunionyesha?”

    “Ndio mkuu. Hao watu watatu wamejirudia. Ni watu ambao wamefanya tukio zaidi ya moja sasa nchini. Nadhani ni muda muafaka wa kutangazwa ulimwengu mzima kama magaidi.” Mwanamama alimimina maneno bila kumung’unya mung’unya.

    Zilikuwa na picha tano, sura ya Amadu ikijirudia kwenye kila picha, wakati sura ya Chui na Talib zikijirudia mara mbili na Mohamed yeye pekee akiwa katokea mara moja. Mkuu alizitizama kwa umakini zile picha kisha akamwambia mwanamama;

    “Fanya hivyo kama ulivyosema, haraka.”

    Mwanamama akaitikia kwa kupandisha kichwa chake. Kikao kikafungwa.







    Baada ya siku tatu tangu tukio la kutekwa kwa watoto lipate kufanyika, picha za Amadu, Talib na Chui zilitandazwa mitandaoni na kwenye kila chombo cha habari cha Sierra Leone huku dau nono likitangazwa kwa yeyote atakayefanisha kukamatwa kwa magaidi hao wa MDR.

    Zaidi ya hapo, ikiwa ni kwa chini chini, serikali ya Sierra Leone kwa kupitia wakubwa wa jeshi wakawateua wanaume makomando saba kwa ajili ya tukio la kwenda kuvamia nchini Guinea kutafuta na kuvamia kambi ya waasi wa MDR. Makomando hao wakakutana na kupewa maelekezo. Wakahaidiwa kulipwa pesa nzuri kama wangelifanikisha kile walichotumwa.

    Basi yakawa hayo. Ilipohitimu siku ya nne rasmi tangu watoto wa shule watekwe, makomando wakajitwika kila aina ya silaha wakaanza safari kuelekea walipotakiwa kwenda kutimiza walichoagizwa.

    Huko nchini Guinea ndani ya kambi ya MDR, hakuna hata aliyeotea nini kitatokea siku hiyo ndani ya masaa machache yajayo. Shughuli zilikuwa zinaendelea kama kawaida, wengine wakifanya mazoezi na wengine wakifanya kazi kama vile kukata kuni, kuchimba mashimo ya choo na kadhalika. Amadu, Chui na Farah walikuwa pembezoni ya mto wakiwa wanafua nguo zao za kijeshi, mwilini walikuwa wamevalia nguo za kiraia, Amadu alikuwa kavalia bukta fupi ya kaki na shati jeupe jepesi, Chui alikuwa kavalia kaushi na bukta iliyokatwa toka kwenye suruali nyeusi ya kitambaa na Farah alikuwa kavalia kaushi nyeusi na suruali kavu ya jeans iliyochoka.

    Wakati wakifua, walikuwa wanaongea habari za hapa na pale ila hasa juu ya ishu ya watoto wale waliotekwa. Amadu akionekana bado kutopendezwa na lile jambo.

    “Mazoezi wanayowafanyisha wale watoto ni makali mno ukilinganisha na umri wao, nadhani general inabidi aambiwe.” Amadu alisema huku akifikicha nguo zake. Farah akatikisa kichwa.

    “Unadhani italeta mabadiliko yoyote? … General anafahamu kinachoendelea. Na hakuna linalofanyika pasipo yeye kuruhusu.”

    “Mmmh mmh. Lazima lifanyike jambo, Farah. Wale watoto wanakula mlo mmoja tu. Kuanzia asubuhi mpaka jioni wanafanya mazoezi, si kuuana huko? Tena mazoezi makali.”

    “Ni kumshauri tu, general, anaweza akaelewa.” Chui alichangia.

    “Tatizo ni kwamba, hakuna chakula cha kutosha stoo kuwalisha watoto wote wale. Najua hilo, sasa si tumeleta kuja kuwaua watoto wa watu!” Amadu alifunguka, akisema kwa mjazo.

    “Tatizo mkuu ametaka kusolve tatizo kwa haraka bila kutazama kama anatengeneza tatizo jingine tena kubwa tu. Sasa hawa watoto watatufia huku. Jana tu yenyewe wamekufa watatu, ona.” Farah alisema.

    “Sasa angefanyaje?” Chui aliuliza.

    “Angetuliza kichwa zaidi. Hakutakuwa kukurupuka. Naona tunawaumiza tu wenzetu wasio hata na hatia. Huoni kama tunatengeneza mduara wa visasi?” Amadu aliuliza.

    “Ni kweli.” Chui akajibu. Farah akaongezea;

    “Unachokiongea kina ukweli ndani yake. Ila sasa hatuna la kufanya.”

    “Hapana. Lazima liwepo. Ni kitendo cha muda tu.” Amadu alifafanua. Hakuna tena aliyeongea, malalamiko ya maji tu ya mto ndio yakawa yanasikika. Walimaliza kufua wakawa wanasuuza sasa. Na hapo ndipo wakasikia mlio wa risasi kwanguvu.

    “Imetokea wapi hiyo?” Farah aliwahi kuuliza. Chui akanyooshea kidole muelekeo wa kambini na kusema;

    “Watakuwa wanafanya mazoezi hao.”http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    “Mazoezi na bunduki za ukweli? Leo sio siku ya kulenga shabaha.” Amadu alieleza. Mara milio ya risasi ikaanza kufululiza kama matone ya mvua. Amadu na wenzake walificha nguo zao wakaanza safari kurudi kambini kwa tahadhari. Hawakuwa na silaha yoyote.

    Kadiri walivyokuwa wanasonga kuelekea kambini, sauti za milio ya bunduki ndiyo ikawa inavuma kwanguvu. Wakaanza kusikia na vilio vya watoto! Walisogea na kusogea, mara wakamuona mwanaume mmoja akiwa ameshikilia bunduki.

    “Tumevamiwa!” Amadu akasema kwa sauti ya chini. Walijibanza kwenye kichaka wakimtizama mwanaume yule aliyekuwa anarusha macho yake huku na huko akielekezea bunduki anapopatizama. Amadu akaokota jiwe kubwa akarusha na kumbamiza kwa nguvu mwanaume yule, ambaye pasipo jadili alikuwa ni komando wa Sierra, mwanaume yule akadondoka chini na kuzirai, Amadu akachukua bunduki wakasonga mbele, bado wakitembea kwa tahadhari kubwa.

    Walipofika kambini wakakuta vita kubwa. Risasi zilikuwa zinarushwa huku na huko, na miili ya wafuasi wa MDR ikiwa imezagaa, michache ya makomandoo wa Sierra Leone. Chui na Farah nao wakatwaa bunduki, wakaendeleza mapambano. Walitumia utatu wao vyema kwa kujilinda na kushambulia. Walitengeneza kamduara wakipeana migongo, taratibu wakawa wanasogea huku wakishambulia.

    Baada ya dakika kama thelathini, kukawa kimya. Milio ya bunduki ilipumzika. Makomando wote kumi wa Sierra Leone walikuwa chini. Kengele ya wafuasi wa MDR iligongwa, wote waliokuwa hai wakakutana eneo moja la makutano. Kessy akasimama mbele yao.

    “Tumeshambuliwa na wanajeshi wa Sierra Leone, mpaka sasa tumepoteza wenzetu hamsini kamili. Ni loss kubwa mno. Zaidi ya hapo, tumepoteza watoto kumi na mbili kati ya arobaini walioletwa. Nayo pia ni loss kubwa. Tunachohitaji ni kuwa pamoja katika kipindi hiki kigumu, na tamko toka kwa mkuu litatolewa muda si mrefu. Kwa sasa, twende tukawapumzishe wenzetu.”

    Baada ya tamko hilo, miili ya wafuasi wa MDR waliokufa ikabebwa na kwenda kuzikwa. Kama ilivyo ada wakati wa maziko, nyimbo za mapinduzi zikawa zinaimbwa. Machozi yalishuka kwenye baadhi ya macho ya wafuasi hao. Zoezi lilipokamilika, wote wakawapa migongo wafu na kuondoka zao.

    Baadae mida ya jioni jua likielekea kuzama, Assessoko akaja kambini kukutana na General Kessy. Uso wake ulikuwa umejikunja, kabla hata hawajapeana salamu, alibamiza meza kwanguvu na ngumi yake kubwa. Kessy akaanza kuelezea;

    “Ilikuwa ni shambulizi la kushtukiza, mkuu. Hakukuwa na jinsi.”

    “Hakukuwa na jinsi hatutuokoa na kuangamia, Kessy! Ina maana mfumo wenu wa ulinzi haupo sawa. Inakuaje mnastukizwa na kuuwawa hivyo!”

    Kessy akatizama chini asiseme jambo.

    “Hapa unavyoniona nimetoka kuonana na raisi wa Guinea, hataki kutuona nchini kwake tena. Vyombo vyote vya habari vinaisakama serikali yake kwa kuwaficha waasi. Si siri tena! Hakuna tena mjadala, wote kesho tunahamia Kabala!”

    “Sasa mkuu, vipi kuhusu hawa watoto? … Nao watapelekwa huko?”

    “Hapana. Mateka tutakwenda nao, ila watoto watabaki huku chini ya jeshi la Guinea. Kessy, mpaka sasa hatujapiga hatua yeyote kuonyesha tunataka kuuchukua utawala wa Sierra Leone. Tumeganda pale pale, hatuna madhara kabisa! … Simaanishi madhara kama haya ya kuteka watoto, la hasha, madhara makubwa. Nadhani sasa ni wakati wa kuwa na madhara makubwa. Le tueurs wa Liberia wanatushinda. Mpaka sasa wameshaweka karibia nusu na robo ya Liberia, kwanini sisi tumeganda hapo hapo? Wafadhili wetu wamekuwa wagumu kutoa pesa kwakuwa hawaoni tena impact. Inabidi tuwape sababu ya wao kutuamini sasa.”

    “Sawa, mkuu. Nimekuelewa.”

    Assessoko alishusha pumzi ndefu akakuna kidevu chake.

    “Kuna vijana wangu watatu nimewaona kwenye runinga wanatafutwa. Wako wapi?”

    “Wapo mahemani mwao.”

    “Naweza nikawaona. Inaelekea ni watu wa kazi sana. Maelezo yao yanayotolewa kwenye vyombo vya habari yanaonyesha wana uwezo mkubwa.”

    “Acha niwaite.”

    Punde, Amadu, Chui na Talib wakawepo ndani ya makao. Assessoko akawapongeza kwa kazi waliyoifanya lakini pia akawapandisha vyeo na kuwafanya wawe makamu wakuu, watu ataokuwa anaonana nao baada ya General Kessy.

    “Unaju mtu akifanya jambo kubwa lazima apongezwe. Huyu Kessy mnayemuona hapa, yeye ndiye alikomboa uhai wangu toka kwenye mikono ya mshenzi mdhalimu Louis Diarra. Alikubali kujitolea uhai wake, akakaa mbele yangu akiwa na bunduki akawamaliza maadui. Bila yeye nisingalikuwepo hapa. Na ndio mana nikaamua kumpa hii nafasi aliyopo sasa. Anastahili. Na nyie nimeona juhudi zenu. Mnastahili. Na mkifanya makubwa zaidi ya haya, mtapata mengi zaidi. Sawa?”

    “Sawa, mkuu.”

    Amadu na wenzake wakaondoka na kumuacha Kessy na Assessoko ambaye naye punde aliaga akaondoka zake. Mkutano ukaitishwa wa wafuasi wa MDR, maamuzi yote ya kikao cha Kessy na na Assessoko yakaekwa wazi.

    Jua lilpochomoza, ndani ya nchi ya Sierra Leone, kukaitishwa kikao. Watu wale wale waliopanga kuvamia Guinea kwa kutumia makomando, walikutana kwa mara nyingine.

    “Kuna taarifa yoyote jamani?” Mwanaume aliyevalia suti aliuliza.

    “Hakuna, mkuu. Tangu tulipopata maelezo kwamba wameshafika eneo la tukio, hatujapata kingine mpaka sasa.” Mjumbe mmoja akachangia.

    “Watakuwa wameshauwawa.” Mwingine naye alisema.

    Mwanaume ndani ya suti akashusha pumzi ndefu.

    “Hilo ni tatizo sasa. Haiwezi ikaleta ngwengwe huko Guinea endapo ikijulikana ni wa Sierra?”

    “Hapana, sidhani.” Mwanamama wa kikaoni alisema.

    “Kwanini?” Mmoja wa wajumbe akauliza.

    “Kwasababu endapo wakifanya hivyo, watatengeneza headline. Swali litakuja, kwanini wanajeshi wa Sierra waende huko. Na itazidi kuongeza nguvu kwenye mwangwi wa taarifa kwamba kuna kitu Guinea, na hata kukamata attention ya vyombo vya habari vya nje.”

    “Vipi kama raisi wa Guinea ataliongelea katika sura ya uchokozi wa kivita?” Mjumbe akauliza. Mjumbe mwenzake akajibu;

    “Hawezi. Anajua kama akianza mashambulizi dhidi yetu, ulimwengu mzima utakuwa upande wetu. Hawezi akashinda!”

    “Ok … Ok … Embu tuachane na hayo. Jana maombi yalikuja mezani kwa raisi yakitokea Liberia. Wanaomba msaada wetu wa kijeshi, wamezidiwa na kundi la waasi la Le tueurs. Mnalionaje hili?” Mwanaume mwenye suti alifungua uzi mpya.

    “Hatuwezi kuwasaidia kwa sasa japokuwa kweli wana mahitaji. Kumbuka na sisi tupo katika wakati mgumu pia.” Mjumbe mmoja alichangia, wenzake wote wakamuunga mkono ya kwamba haiwezekani.

    “Sawa, nadhani sasa ni wakati muafaka wa kujadili nini cha kufanya kwa muda huu na hali tuliyopo. Nakaribisha mawazo yenu.”

    “Mkuu, nadhani huu ni muda muafaka kwa mheshimiwa kuomba msaada mataifa ya magharibi. Endapo kama tutafaulu katika hilo, tutakuwa tumeukata mzizi wa fitna kabisa.” Alisema mjumbe.

    “Tatizo kuomba msaada kwa hayo mataifa inakuwa ngumu kwetu kutokana na njia ambayo raisi wetu ameingilia madarakani. Marekani na uingereza wanamuona Diarra kama gaidi kwao. wapi unadhani tutapata msaada?” Mjumbe mwingine alitia neno.

    “Kama marekani na waingereza hawapo tayari, mi naona tuwafuate warusi tu. Wanaweza wakatusaidia. Naamini hilo.” Mjumbe mwingine akachangia.

    “Sawa. Nitayafikisha mawazo yenu.” Mwanaume aliyevalia suti alinena. Kikao kikafungwa.

    Usiku ulikuwa tayari umeshaingia.

    Wasaa ulikuwa ni saa nne inayoitafuta saa tano ya usiku. Amadu alikuwa amejilaza kitandani kwake yeye na Chui. Usingizi ulikuwa umempitia lakini Chui yeye alikuwapo macho. Alikuwa anatizama dari kama vile kuna jambo fulani analitafakari.

    Baada ya muda kidogo, Amadu alipata njozi. Alijiona akiwa msituni yeye pamoja na Chui, Farah, Mou, Ussein na Ulsher. Walikuwa wakikimbia wakielekea kaskazini huku nyuma yao milio ya risasi ikirindima. Ila ghafla, bomu lilishuka mbele yao na kuwalipua vibaya mno. Wengine wote walichanwa na kupasuliwa na bomu akabaki yeye tu tena akiwa chini anagugumia maumivu ya hatari. Alikuwa hawezi kusogea maana miguu imeharibika. Damu zilikuwa zinamvuja mno. Mara, General Kessy akatokea mbele yake akiwa kabebelea bunduki. Alisogea karibu akanyooshea mdomo wa bunduki kwa Amadu. Alipofyatua, Amadu akashtuka toka usingizini!

    “Nini Amadu?”

    Chui aliuliza kwa tembe ya hofu. Amadu baada ya kutizama kushoto na kulia kwake, akashusha pumzi ndefu na kutikisa kichwa.

    “Nimeota ndoto ya ajabu!”

    “Ndoto gani?”

    Amadu alitulia kwanza kama vile anatafakuri. Alijifuta jasho na kiganja chake, akamtizama Chui.

    “Nimeota tupo mahali tunatoroka mimi na wale wenzetu tulioenda nao ile mishe ya Liberia pamoja na yule mdada mateka. Tukiwa njiani bomu likarushwa nisijue hata limetokea wapi, likatusambaratisha vibaya mno. Wakati nikiwa najikongoja kuamka, akatokea general akaninyooshea bunduki. Ile kufyatua tu ndo’ kushtuka!”

    “Mmmh … Mbona ndoto yako inantisha? … Tulikuwa tunaenda wapi?”

    “Hata sijui wapi tulipokuwa tunaelekea. Sielewi! Unadhani itakuwa ina maana gani hiyo ndoto?”

    “Sijui!”

    Amadu alinyanyuka akatizama saa yake ya mkononi akaona ni saa sita kasoro vidakika kadhaa. Alitupia shuka kando akaufuata mlango wa hema lao.

    “Wacha ninyooshe miguu, naenda chimbo mara moja.” Amadu alimuaga Chui kisha akatoka na kuelekea zake chimboni. Alimkuta Ulsher amelala, na hata mzee Buruwani pia. Ila vishindo vyake vya miguu vikamshtua mzee Buruwani, akaamka na kutizama. Amadu akafungua mlango na kuingia ndani.

    “Unaendeleaje, mzee?”http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    “Naendelea vyema.”

    “Umekula leo?”

    “Ndio, nimekula baba.”

    Amadu aliketi chini akamtizama mzee Buruwani.

    “Umetokea wapi, mzee? Na ulikuwa unafanya nini?”

    “Nimetokea Kankan na shughuli yangu ni ukulima, baba.”

    “Una familia?”

    “Ndio. Mke na watoto watatu. Wote wanaishi huko Kankan huku huwa nakuja kwa ajili tu ya kilimo.”

    “Ilikuwaje ukaingia katika haya matatizo?”

    “Nilikuwa tu namsaidia yule binti. Nilisikia kwenye karedio kangu kwamba kuna zawadi kwa atakayetoa taarifa.”

    Amadu alitikisa kichwa chake kwa masikitiko akatizama chini. Alitizama kushoto na kulia kwake akamwambia mzee Buruwani.

    “Ukitoka hapa unaweza ukaenda mpaka nyumbani kwako?”

    “Ndio! Naweza!”

    “Utaufunga mdomo wako huko utakapokwenda?”

    “Nakuahidi kwa roho yangu. Sitasema jambo!”

    Amadu alimtizama mzee Buruwani kwa macho ya huruma. Akatoka nje na kutizama pande zote zimzungukazo. Alipoona ni shwari, akarudi chimboni na kumfungulia mzee Buruwani.

    “Pita njia hii ya mashariki. Kwa mbele kidogo utaona imekata kona, usiende nayo, wewe nyoosha mpaka ufike mtoni na uendelee na safari yako. Ukipita mbali na maelekezo yangu utaakutana na walinzi, utauwawa.”

    “Sawa.”

    “Angalia wanyama wasikudhuru.”

    “Ahsante. Nakushukuru sana mwanangu.”

    Mzee Buruwani akashika njia na kuondoka. Amadu alimtizama mpaka anapotelea kisha akarudi zake hemani. Alimkuta Chui kalala, naye alipojilaza tu kitandani Chui akaamka.

    “Nimemwachia yule mzee aondoke.”

    “Buruwani?”

    “Ndio.”

    Chui kusikia hivyo akanyanyuka na kuketi kitako.

    “Kwanini?”

    “Sijaona haja yay eye kukaa humo. Ana familia inayomtegemea na anatakiw awe nayo.”

    “Vipi akienda kutoa taarifa?”

    “Hatosaidia chochote. Kesho wote tunaenda Kabala, Sierra Leone. Taarifa yake itasaidia nini?”

    Ukimya ukashika anga kwa sekunde kadhaa. Chui akauvunja kwa kuuliza;

    “Lakini vipi mkuu akijua?”

    “Hatoweza kujua. Hata kama akijua, nitawajibika kwa nilichokifanya kwani naamini ni sahihi.”

    Walilala usiku ukapita. Taa ya mungu ilipomulika kengele ikagongwa na wafuasi wote wa MDR waliobakia wakakusanyika. General Kessy akasimama mbele ya umati na kutangaza siku ile ni siku ya kuondoka kwenda mji wa Kabala, hivyo wote wakajiandae kufanya zoezi hilo, umati ukatawanyika.

    Baada tu ya muda mfupi yalikuja magari manne aina Fuso yasiyo na namba za usajili, yakapaki kwenye uwanja wa kambi. Magodoro, mahema, vyombo na mabegi yakapakiwa humo, hata watoto waliotekwa nao wakaswagwa humo chini ya uangalizi wa wanajeshi kadhaa. Watu walijiweka tayari, wakapanda kwenye magari ya mapambano ya MDR wakawa wanangoja tu amri toka kwa mkuu waende. Amadu pamoja na Chui wao walijipaki kwenye lile basi lao.

    General Kessy alitoka kwenye hema lake akiwa anaongozana na mfuasi wake mmoja aliyekuwa amebebelea bunduki begani. General alionekana ameghafirishwa na jambo, uso wake ulieleza kwa ndita na hata matendo yake aliyokuwa anafanya pindi anaongea.

    “Nyie mlikuwa wapi?”

    “Tulikuwa lindoni kama kawaida, mkuu.”

    “Sasa mateka anatorokaje kizembe hivyo?”

    “Sisi wenyewe hatujui, mkuu. Hatujui ametokaje ndani ya chimbo.”

    “Hamjui! Kazi yenu ilikuwa ni nini? Kuzurura?”

    “Hapana, mkuu!”

    “Kwa huo uzembe tutashika dola kweli?”

    Kimya.

    “Na mtoto wa waziri?”

    “Huyo yupo, tumeshampaki kwenye gari.”

    “Ok. Twendeni! Ila mkifika lazima muwajibishwe.”

    Mpaka wanamaliza hayo maneno walikuwa tayari wameshayafikia magari. General alipanda gari lake binafsi akiwa na dereva wake, safari ya kuelekea Kabala ikaanza.

    Baada ya mwendo wa masaa matano wakawa tayari wamekwishaingia mji wa Kabala, nchi ya Sierra Leone baada ya kuteketeza kilomita 255 njiani. Walipokelewa na wenzao kwa shangwe na nderemo. Mizigo ilishushwa, makazi ya mahema yakatengenezwa kwa ajili ya wakazi wapya.

    Siku moja ikapita.

    Siku iliyofuata, mkutano uliitishwa na General Kessy akahutubia umati kuwaweka wanajeshi wake katika utayari wa mashambulizi makubwa kuanzia siku ile kamili. Hakuna tena muda wa kupoteza, ni wakati wa kuleta madhara makubwa katika nchi ya Sierra Leone. Baada ya mkutano huo, General Kessy akawaita Amadu na Chui ofisini kwake, akawapa kazi;

    “Jeshi la Sierra Leone limefungua kambi dogo maeneo ya Makeni. Wamefanya hivyo kwa ajili ya kurahisisha kazi yao ya kuurudisha mji wa Kabala. Sasa nataka mkafanye kazi huko kwa kuteketeza kambi hiyo ndogo yenye vifaa vya kila aina. Chagueni wenzenu mkaitende hiyo kazi sasa hivi.”

    Amadu na Chui wakaridhia. Walichagua watu wao watatu na muda ukapangwa wa kwenda kufanya tukio, saa nne za usiku.

    General akamuita Talib ofisini, naye akampa kazi yake;

    “Ndani ya siku ya leo, nataka muende Magburaka. Kazi yenu kuu ni kutekeza tu, kuanzia ofisi za serikali, mpaka watu! Hakuna kuleta huruma, nataka nisikie taarifa ya habari leo za mauaji. Nataka leo serikali ya Sierra ijue ni jinsi gani tuna maanisha. Chagua watu wako, mkaitende kazi.”

    Talib akaridhia. Alichagua watu wake kumi na mbili na muda ukapangwa wa kwenda kufanya tukio, saa kumi ya jioni.

    Sasa ilibakia saa tu kuamua mambo hayo mawili. Ilipofika saa tisa ya jioni, magari manne yakatoka kambini yakiongozwa na Talib kuelekea Magburaka. Saa moja ya usiku ilipohitimu, yakatoka tena magari mengine mawili yakiongozwa na Amadu kuelekea Makeni, ndaniye walikuwepo Ussein, Mou, Farah na Chui.

    Kila kitu kilienda kama kilivyopangwa. Kambi ya Makeni iliteketezwa na hata silaha zikabebwa. Wakina Talib waliteketeza kila ofisi na walimimina risasi za kumwaga mitaani wakaua watu mia moja na mbili, wakiwemo wamama na watoto. General alifurahishwa sana na hayo mafanikio. Mipango mingine ikaanza kusukwa.

    “Soko kuu na ofisi za mji wa Bo, pamoja na mji wa Kenema vinatakiwa kufanyiwa mashambulizi ndani ya kesho kutwa. Hatuna muda wa kupoteza. Mtajigawa makundi mawili, moja litakwenda Bo na lingine Kenema. Kundi la Kenema litaanza kushambulia kwanguvu, wakati majeshi ya Sierra yakitumwa kwenda Kenema, kundi la Bo litaanza nao kushambulia kwanguvu, sawa?”

    General alimpa maelekezo Talib na wenzake kumi na mbili. Wakapokea maelekezo na kwenda. Amadu na Chui wakaitwa.

    “Keshokutwa nataka muende Freetown. Kazi yenu kubwa ni kuhakikisha mnateka maofisa wa serikali, nataka mniletee mawaziri ama manaibu waziri hapa, ama mkuu wa mikoa. Tumeelewana?”

    “Ndio, mkuu.” Amadu na mwenzake wakaitika.

    Baada ya siku moja kupita, ikafika siku ya tukio. Talib na wenzake walijitwika kwenye magari yao, safari ya kuelekea kwenye maeneo ya matukio ikaanza. Walijigawa makundi mawili kama walivyopangwa. Wakina Amadu wao walinyooka na njia kwenda Freetown.

    Mpaka muda ambao jua lataka kupumzika, makundi yote yakawa yameshawasili maeneo yao ya kazi. Amadu akiwa na wenzake wa kazi walifikia nyumba moja ya mapumziko huku Amadu na Chui wakiwa wamevalia kofia na miwani kuficha nyuso zao. Wakiwa hapo chumbani wakaanza kupanga mipango yao ya mashambulizi. Waliamua kuanza na ofisi ya mkuu wa mkoa. Waligawana majukumu, na kila tukio likachorwa kwenye karatasi.

    “Mou utakwenda na kuingia ofisini. Utabebelea bahasha na kudai una mahitaji toka kata yako na wilayani wamekuambia uende ofisi ya mkoa. Hakikisha unakuwa serious na unahakikisha unaonana na mkuu wa mkoa na unamweka kwenye himaya yako. Muda huo wote utakuwa unawasiliana na sisi kwa kupitia micro mic tutakayokufungia.” Amadu alieleza.http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    “Sawa.” Mou akajibu.

    “Taarifa zako ndizo zitatupa sisi nafasi na jinsi ya kujipanga.”

    “Haina shida.”

    Baada ya kupanga, wakapumzika kwa usingizi. Amadu yeye alikuwa macho. Alifungulia runinga akawa anatizama. Kwenye kituo kimoja cha runinga akawa anaona matangazo moja kwa moja juu ya kinachotukia huko mji wa Kenema, wananchi mia mbili na ushee wameuwawa na watuhumiwa ni kundi la MDR.

    Amadu alinyanyuka akaa kitako apate kuona vizuri. Macho yake yote yalitilia maanani akionacho na punde tu yakaanza kujaa machozi. Aliona maiti zikiwa zimezagaa, watoto wakilia kwa kupoteza wazazi na hata watu wazima pia wakilia kwa kupoteza familia zao. Moja kwa moja akaanza kukumbuka machafuko yaliyowahi kuikumba nchi ya Sierra Leone, jinsi alivyopoteza wazazi wake na dada yake. Kila aliyemuona runingani akiwa anaongea huku analia akajiona ni yeye ndiye analonga. Hata sauti hakusikia tena, alisikia sauti ya Ulsher ikimuita na kumshutumu ya kwamba ni muuaji wala si mwanamapinduzi. Alihisi kuchanganyikiwa, mwishowe alizima runinga akalala.

    Asubuhi ya saa moja inayoitafuta saa mbili, Amadu aliamshwa na Chui akatakiwa ajiandae kwa ajili ya tukio walilopanga jana. Amadu akaamka na kuuliza;

    “Mou amekwisha kwenda?”

    “Ndio!” Chui alijibu, “amekwishaingia kwenye jengo la mkoa, anasubiria sasa mapokezi. Ametuambia kuna ulinzi mkali.”

    “Umemwambia asiue mtu?”

    “Si tulishakubaliana tokea jana. Sasa amka ujiandae tuondoke. Kwa sasa tunatakiwa tuwe maeneo ya karibu na ofisi ya mkoa.”

    Amadu alikuwa kama mtu mwenye bumbuli la mawazo. Picha za mauaji alizoziona jana kwenye runinga bado zilikuwa zinamtafuna akili. Farah alimpiga kofi la mgongo kumshtua.

    “Mbona kama una mawazo?” Farah aliuliza.

    “Vipi, haupo sawa?” Ussein naye akaongezea.

    Amadu alitikisa kichwa chake kujirudisha fahamuni. Alinyanyuka akaenda kunawa uso, ni yeye peke yake ndiye aliyekuwa yupo nyuma kwa kujiandaa. Aliponawa walitoka ndani ya chumba wakajipakia kwenye gari lao na kusogea maeneo ya karibu na ofisi ya mkuu wa mkoa. Wakaendelea kuwasiliana na Mou aliyekuwepo ndani.

    “Naweza nikakusaidia shida yako?” Mwanamke mmoja mnene mweusi alimuuliza Mou aliyekuwa kwenye benchi.

    “Nataka kuonana na mkuu wa mkoa.”

    “Hata mimi naweza kukusaidia. Naomba unijuze shida yako.”

    “Nimesema nataka nionane na mkuu wa mkoa. Mara ngapi nimekuja hapa na hamkusaidia? Nataka kumuona mkuu wa mkoa nimueleze shida ya kata yangu macho kwa macho.”

    “Kwani wewe ni nani, kaka?”

    “Diwani.”

    “Sasa si ungeenda wilayani kwanza.”

    “Nimeshaenda mara kibao, wazembe tu. Nalalamika kila uchwao kuhusu swala la maji naona sieleweki. Nimekuja kwa mkuu wa mkoa mwenyewe.”

    “Unatoka kata gani?”

    “Mbona maswali mengi, dada? Nataka kuonana na mkuu wa mkoa. Nataka anieleze kwanini wakina mama kwenye kata yangu wanapata shida ya maji hivi? Watoto hawaogi, hawaendi shule, watu wanakufa kwa kiu!”

    Watu wengine waliokuwa wamekaa karibia na Mou wakamuunga mkono. Walionekana kuguswa na anachokiongelea Mou, diwani feki.

    “Ila kaka, unajua matatizo ambayo yanayoikumba serikali kwa sasa, pesa na rasilimali nyingi zimeelekezwa kupambana na waasi. Kununua masilaha na kuwapa wanajeshi motisha.” Mwanadada alieleza.

    “Kwahiyo watu wafe?” Mou aliuliza.

    Maongezi yote hayo wakina Amadu waliokuwepo kwenye gari wakawa wanayasikia. Walikuwa wametulia tuli wakiacha masikio yao yafanye kazi kwa umakini. Gari lao lilikuwa umbali wa kama hatua thelathini za mtu mzima toka ofisi ya mkuu wa mkoa. Walikuwa wamelizima kabisa ili wapate kudaka kila habari.

    Miongoni mwa wanajeshi waliokuwa wanalinda eneo la ofisi ya mkuu wa mkoa walilitizama gari la wakina Amadu na kulitilia shaka. Si kwamba halikuwa na namba ya usajili, la hasha. Ila kuwapo kwake pale maeneo ya ofisi kubwa kama ile bila ya kuonekana na shughuli yoyote kulizua hofu.

    “Embu katizame lile gari pale, afande. Naona limekaa kwa muda na sioni mtu yeyote akishuka wala kufanya lolote.”

    Alisema mwanajeshi mmoja akimuambia mwenzake. Mwenzake akatii, akiwa kabebelea na kushikilia bunduki yake akasogelea gari la wakina Amadu na kugonga kioo. Kong! Kong! Kong!

    Kioo kilishushwa uso wa Ussein ukajitokeza.

    “Ndio, afande.”

    “Una ajenda gani hili eneo?”

    “Kuna mtu namngoja.”

    “Nani?”

    “Mheshimiwa diwani, ameingia huko ofisini.”

    “Upo na nani ndani ya gari?”

    “Peke yangu, afande. Kuna tatizo?”

    “Embu nione.”

    Ussein alishusha vioo vyote mwanajeshi akapepesa pepesa macho yake ndani, aliporidhika akasema;

    “Huyo mtu unayemngoja anatoka saa ngapi?”

    “Sijajua, afande. Sijui michakato gani anayopitia huko.”

    “Hili ni eneo muhimu la serikali. Haitakiwi kuonekana onekana kwa magari yakiwa yamesimama simama bila ya taarifa. Sasa nakupa dakika kumi tu, kama huyo diwani wako atakuwa hajatoka inabidi utoke hii sehemu. Tumeelewana?”

    “Ndio, afande.”

    Mwanajeshi alijigeuza akarudi kumkuta mwenzake na kumpasha habari alizozipata. Amadu, Farah na Chui walitoka chini ya viti vya gari wakarusha rusha macho yao kutazama usalama.

    “Sasa itakuaje? … Mou amekupa taarifa yoyote?” Farah aliuliza.

    “Hapana, ila amekwishaingia ofisini kwa mkuu wa mkoa.” Ussein alisema kisha akatoa earphone ya sikio la kulia akampachikia Farah sikio la kushoto.

    “Inabidi afanye upesi. Hatuna tena muda wa kukaa hapa.” Amadu alisema. Ussein akasogeza mic ndogo mdomoni mwake;

    “Mou fanya upesi, hatuna muda.”

    Baada tu ya dakika tangu Ussein atume huo ujumbe, sauti ya Mou ikasika kwanguvu.

    “Ingia! … Ingia! … Nimeshamuweka mkuu wa mkoa chini ya ulinzi!”

    Haraka Ussein aliwasha gari, kwa mwendokasi mkali wakavamia geti, Amadu, Chui na Farah wakatokezea madirishani na kuanza kumwaga vyuma vya risasi wakiwalenga wanajeshi waliokuwa lindo.

    “Usiue raia yoyote! Usiue raia yoyote!” Amadu alipaza sauti huku naye akishughulika kuwamiminia walinzi risasi. Gari lao lilizunguka jengo zima huku risasi zikirindima kisha kila upande wa jengo akashuka mtu mmoja kufanya kazi: Upande wa mbele alishuka Amadu, wa nyuma alishuka Chui na wa pembeni akashuka Farah. Mou alitoka akiwa kamkaba mkuu wa mkoa amemkandamizia bunduki, wanajeshi hawakuweza kumshambulia, waliweka bunduki chini wakanyoosha mikono yao juu. Mkuu wa mkoa aliwekwa ndani ya gari, wakina Amadu wakawamalizia wale wanajeshi kwa risasi, wakapasua na matairi yote ya magari yaliyokuwepo yale maeneo kisha wakaondoka.

    Hata taarifa zilipokuja kusambaa kuhusu utekaji, wakina Amadu walikuwa wapo mbali mno. Walikuwa wanabadili gari kila baada ya muda mchache kwa usalama wao, walimfunga mkuu wa mkoa kamba na kumziba mdomo wakawa wanamuweka kwenye buti kwenye kila gari walilolitumia mpaka wanafika Kabala. General Kessy aliwapokea kwa mikono mikunjufu na tabasamu pana. Ila Amadu hakuwa na furaha, baada tu ya kumkabidhi mateka, aliondoka zake.

    “Vipi, kuna tatizo?”

    General Kessy aliwauliza Chui, Farah, Mou na Ussein.

    “Hapana. Hamna!” Farah alijibu.

    “Mbona Amadu ameondoka na anaonekana hana furaha?”

    Wakina Chui walitazamana, Farah akajibu;

    “Hatujui kwanini.”

    General Kessy aliwaruhusu waondoke, Chui akamfuata Amadu hemani. Alimkuta akiwa ametulia, uso wake mkunjiko ukiwa umeelekea chini.

    “Amadu, shida nini?”

    Amadu alishusha pumzi ndefu kwa kutumia matundu ya pua yake kisha akamtizama Chui.

    “Sisi si wanamapinduzi bali wauaji.” Alisema kwa sauti iliyobeba hisia.

    “Kwanini unasema hivyo?”http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    “Kwanini? … Huoni, husikii jinsi MDR inavyoua watu wasio na hatia: wanawake kwa watoto? Wametufanya kosa gani? Je tutakapoingia madarakani hawatakuwepo wakina sisi wengine wakidai damu za ndugu, jamaa na marafiki zao? … Jana nilitizama taarifa ya habari kule tulipopumzikia, niliona jinsi maiti zilvyozagaa, watoto na watu wazima wakilia huko Kenema na Bo. Nikajikumbuka mimi kabisa. Nikakumbuka yale niliyoyapitia.”

    Chui alikaa kitako kitandani akatulia kwa muda, alimshika Amadu bega akamuambia;

    “Pole sana. Najua unachokiongea, ni ukweli mtupu. Lakini sasa tutafanyeje?”

    Amadu alinyanyuka akatizama dari. Machozi yalianza kumbubujika kama maji. Aling’ata lips zake akamuambia Chui:

    “Nitakuambia nini cha kufanya. Kwanza, naenda kwa general na kumweleza msimamo wangu.”

    Chui hakupata nafasi ya kutia neno kwani Amadu alitoka upesi hemani akaelekea upande ilipo ofisi ya General Kessy. Chui alitoka nje ya hema akamtizama Amadu anavyoishia, alishika kiuno akatikisa kichwa chake. Akabakia palepale aone nini kitatukia. Baada ya muda mfupi, sauti ya General Kessy ilisikika ikiita wafuasi wa MDR waliokuwa wamekaa nje ya hema. Wafuasi wakaingia ndani upesi na mara wakatoka na Amadu huku wamemshika mikono wakimburuza. Amadu alikuwa anatapatapa lakini wanaume wanne waliokuwa wamemshikilia walimmudu.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog