Search This Blog

Sunday 20 November 2022

NJIA NYEMBAMBA - 5

 





    Simulizi : Njia Nyembamba

    Sehemu Ya Tano (5)





    “Ile siku nilikabidhiwa barua nipeleke kwa General Kessy. Nilikatazwa kabisa nisiifungue huko njiani na nisimpe mtu yeyote bali General. Kwa utaratibu wetu nilitegemea ule ujumbe ambao upo kwenye barua ungekuja kuanishwa mbele yetu, lakini mpaka tunaondoka ule ujumbe ulibakia kuwa siri, sijui ulibeba ajenda gani ambao hatukutakiwa kuufahamu?”

    “Mmmh … kutakuwa na jambo.” Ussein alipata shaka, “Nadhani tutajua kinachoendelea baada ya kuona ni maamuzi gani atakayochukua General Kessy kwenye hili vuguvugu la Liberia.”

    “Kweli.” Wote walikubali kilichosemwa. Mara mlango wa sebule ulifunguliwa akaingia mama mmoja mzee, alikuwa kajivika baibui na kuacha uso pekee ambao ulikuwa unafanana na uso wa Chui mno, kwa mtu anayemfahamu Chui hawezi akapata shida kubashiri kwamba yule alikuwa mamaye.

    “Amir!” Mama aliita jina halisi la mwanae, Chui akamtizama mama na kuitikia,

    “Naam.”

    “Picha zenu zimebandikwa jiji zima la Freetown, mnatafutwa na serikali! … Mungu wangu, mwanangu unaenda kunyongwa!” mama alilia. Chui alitizamana na wenzake pasipo kusema kitu. Mama akaendelea kunena;http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    “Sasa utaendaje kutafuta pesa kwa ajili ya familia na unatafutwa hivyo? Je majirani hawatosema kama upo hapa ili wapate pesa?”

    Chui alinyanyuka akamtoa mama yake kuelekea ndani. Baada ya dakika kadhaa, alirudi mwenyewe, alishika kiuno akashusha pumzi ndefu.

    “Sasa tunafanyeje?”

    “Kaa chini kwanza.” Amadu alimtaka Chui. Chui alikaa akamtizama Amadu.

    “Kitu ambacho mama yako amekuambia ni kitu ambacho tulikuwa tunakitegemea, hakuna haja ya kuogofya. Ni dhahiri MDR wangetutafuta kwa njia yoyote ile. Hapa cha kufanya ni kupanga tujue tunakabili vipi hii hali. Tujue wapi tunatoa pesa, na tufanye uwezekano wa kutoka hili eneo haraka. Kuna yeyote mwenye wazo?” Amadu aliuliza kisha akapepesa macho yake kutizama wenzake, hakuna yeyote aliyesema kitu. Basi Amadu akaendelea kunena;

    “Mimi nina wazo nini tufanye. Na hilo wazo langu litakuwa ni kupiga ndege wawili kwa wakati mmoja, ila lataka utayari.”

    “Amadu, unatuuliza tena kuhusu utayari?” Mou alishangaa. “Sidhani kama kuna ambaye hayupo tayari mpaka saa hii. Yupo?” Mou alitizama wenzake, wote wakajibu;

    “Hayupo!”

    Amadu akaendelea kutema maneno;

    “Wazo langu ni kwenda kuvamia benki kuu ya Sierra Leone. Tunaenda na kubeba pesa za kutosha kukimu mahitaji ya mama yako, na pia kununulia silaha za kufanya mambo yetu. Tutalenga ndege wawili kivipi? Kwanza tutalenga ndege wa kutimiza mahitaji yetu, pili tutalenga ndege wa kudhoofisha serikali ya General Kessy kwa kuiachia hasara kubwa. Mnaonaje?”

    Walitizama kwa sekunde kadhaa chini ya tano, Chui akawa wa kwanza kujibu;

    “Naunga mkono.”

    Wengine wakafuatia; “Tunaunga mkono.”

    Waligusanisha ngumi zao, wakatabasamu.

    “Sasa inabidi tuwe na mipango madhubuti ya kufanya hilo jambo, maana si dogo ni kubwa.”

    “Kweli, Amadu.” Farah alisema, “Inatakiwa tupange kuanzia kutoka hapa mpaka tutakapotoka ndani ya benki. Kila kitu kiwe kimepangwa na si kuendeshwa kwa bahati.”

    “Ni kweli.” Amadu alikubali, “Naomba nifanye hiyo kazi ya kupanga kila kitu. Kuna mjomba wangu anaishi hapa Freetown, ni mhandisi na amehusika sana kwenye kazi ya kuujenga hili jiji tokea kitambo, waziri wa ujenzi alikuwa anampa fursa sana kwakuwa alikuwa ni jamaa yake. Anajua majengo na kila barabara ya huu mji kuanzia barabara za juu mpaka za chini. Atatusaidia sana katika hili.”

    “Sawa, basi utatutaarifu. Au mnaonaje?” Ussein aliuliza wengine, hakuna ambaye alipinga, wakawa wamepeana makubaliano katika hilo. Chakula kilikuwa kimekwisha, Ulsher alinyanyuka akatoa sinia kulipeleka jikoni, akiwa huko anaosha sinia, alisikia redio ikiruruma. Ilikuwa ni redio ya taifa maana ndiyo pekee iliyobakizwa wakati zingine zikiwa zimezuiwa kutangaza. Ulsher aliacha kukosha chombo akatega sikio apate kusikia. Sauti ya mtangazaji ilisema;

    “Muda si mrefu tutajiunga kwa matangazo ya moja kwa moja toka kwa mheshimiwa mkuu wa nchi, amiri jeshi mkuu. Leo hii atatangaza wizara zake na mgawanyo wa majukumu. Hakikisha hukosi tukio hili la kihistoria.” Baada ya hiyo kauli ilifuatia wimbo wa taifa. Ulsher alikosha chombo haraka akabeba redio na kuipeleka sebuleni walipo wenzake. Wote wakatega masikio kusikiliza. Baada ya punde sauti ya General Kessy ilisikika kwenye spika za redio ikisalima wananchi, baada ya hiyo salamu akasema dhamira ya maongezi yake kwa wananchi kuwa ni kutangaza wizara zake na watu watakaozisimamia. Alianisha wizara mbili tu: ulinzi na maliasili, sekta zingine akasema zitaingizwa humo humo ndani ya hizo mbili. Mkuu wa wizara ya ulinzi, akatajwa ni General Talib Awadh na wa Maliasili akatajwa General Mohammed Emmo.

    Bada ya hotuba ya mkuu wa nchi kumalizika, mjadala ukazuka miongoni mwa wakina Amadu.

    “Ana akili kweli huyu mzee, yani anampa wizara Talib? Talib kweli? Hata kusoma na kuandika hajui!” Farah alisema kwa tambo za utani.

    “Cha kushangaza wizara zipo mbili tu, uliona wapi? Na wizara zenyewe, moja ya kumlinda yeye, ulinzi, na nyingine ya kunyonya maliasili za nchi. Hajataja vipaumbele vyake kama serikali, hajatuambia ni kivipi wizara kama ya elimu, fedha, mambo ya nje vinaingiaje kwenye hizo alizotaja.” Ulsher alitanabahi. Amadu naye akatupia yake;

    “Utakuwa ulifanya makosa sana kama ulitegemea mtu ambaye aliacha shule mapema sana tokea utoto wake awe na akili kama hiyo. General Kessy hana ufahamu wowote kwenye mambo ya utawala. Anachojua yeye ni kushika mitutu. Yani ameshindwa hata kutafuta wataalamu, wasomi na wabobezi wamshauri?”

    Amadu aliweka kituo. Kisha akaendelea,

    “Ila kwetu ni faraja. Kuwaweka watu hao kama watu wake wa utawala kunazidi kutupanulia na kutuwekea wazi udhaifu wa serikali hii, itatusaidia kutimiza malengo yetu.”

    “Kweli.” Mou aliwajibia wenzake.













    ********















    Raisi wa Guinea alikuwa amekaa kwenye bustani ya ikulu pamoja na mwanaume mmoja mweusi aliyenyoa mtindo wa panki. Raisi alikuwa amevalia gauni kubwa jeupe la kitamaduni wakati mwenzake akiwa ameficha uchi wake na suti nyeusi. Mbele yao kulikuwepo na ka-meza kadogo ka-mbao kakiwa kamekaliwa na chupa ya maji ya kunywa ikiwa na glasi mbili pembeni. Nyuma yao hatua tano, alikuwepo amesimama mwanajeshi akiwa kabebelea bunduki kubwa, kazi yake ilikuwa kutizama huku na kule uso akiwa kaukunja kama vile amekosana na mtu.

    “Rafiki yangu Kone, nimeumia sana.” Raisi alisema huku akitikisa kichwa, “Nimepata hasara sana juu ya Sierra Leone lakini mwishowe nimeambulia patupu. Wanajeshi wangu wamekufa, baadhi ya vifaa vyangu havijarudi, aisee!”

    “Pole sana, mheshimiwa raisi. Unaonaje kama ukianzisha vita naye, najua hana msaada wowote, ni sisi ndio alikuwa anatutegemea.”

    “Hapana, Kone. Siwezi kuanzisha vita kwa sasa.”

    “Kwanini?”

    “Kumbuka imebakia miezi michache kabla hatujaanza mchakato wa uchaguzi mkuu. Endapo nikianzisha vita nitakuwa najipalia makaa ya kupoteza uchaguzi kwa jambo ambalo halitakuwa na mantiki mbele ya macho ya wananchi. Nitamaliza pesa yote ya uchaguzi. Inabidi niwe na njia mbadala mbali na hiyo.”

    “Nimekuelewa mheshimiwa. Unaonaje kama tukichochea vita ya wenyewe kwa wenyewe alafu sisi tukautumia huo mwanya kufanya yetu?”

    “Tunachocheaje sasa kitu kama hiko na kundi lenyewe la waasi ndilo hilo limeshika dola?”

    “Mheshishimiwa, kuna njia.”

    Kone alisema kwa kujiamini. Alikunywa maji yaliyokuwepo kwenye glasi yake kisha akamtizama raisi.

    “Kuna wafuasi watano wa MDR walioasi kundi lao. Picha zao zimebandikwa maeneo mbalimbali ya jiji la Freetown wanatafutwa kwa hali na mali. Unaonaje kama tukiwekeza kwao?”

    “Kone, unaamini vipi kama hao watu wanaweza kazi mpaka kufikia hatua ya kuwekeza kwao?”

    “Mheshimiwa raisi, nisingependa nikupe jibu la kukurupuka, wacha nikafanye utafiti kwanza. Ila niliguswa nao sana, juhudi kubwa ya kuwatafuta watu hao ilinipa taswira ya kwamba ni watu hatari. Na najua pia hao watu watakuwa wana hamu ya kulipiza kisasi kwa njia moja ama nyingine kutokana na chochote kile kilichowafanya waasi kundi lao.”

    “Sawa, Kone, lakini unajua hili jambo ni sensitive sana. Ningependa ufanye utafiti juu yake kwanza.”

    “Sawa, mheshimiwa. Nitalifanya kadiri ya uwezo wangu.”









    Usiku ulikuwa umeshaambaa kwenye uso wa ardhi ya Sierra Leone. Mwezi ulitawala anga ukionekana vyema kwa ukubwa huku ukiungwa mkono na nyota zilizozagaa kila kona. Ilikuwa ni saa tano ya usiku ikiitafuta saa sita iwe siku nyingine. Amadu pamoja na Ulsher walikuwa wamesimama wakiegemea kuta ya kibaraza cha nje ya nyumba ya wakina Chui. Nyumba nzima ilikuwa kimya na taa zilikuwa zimezimwa kasoro za nje tu. Huko nje kwenyewe kulikuwa kimya, hakuonekana watu wakikatiza, labda vijibwa na paka.

    “Sikuwahi kudhani siku moja nitakuja kufikia hivi kwenye maisha yangu. Kweli hakuna anayeijua kesho yake.” Ulsher alisema huku akitizama nyota zimetazo. Amadu alimtizama akamshika mkono.

    “Najua ni jinsi gani kwako ilivyo ngumu; ulizaliwa na kijiko mdomoni. Lakini usihofu, kila kitu kinachotukia maishani kina makusudi yake, na kinatupa fursa ya kufungua mlango mwingine. Historia ya Sierra Leone haitokuja kukusahau kamwe kwa utakachokifanya.”

    Ulsher alitabasamu. Akamwambia Amadu;

    “Sijawahi kukutana na mtu mwenye moyo kama wewe.”

    Amadu akitizama mwezi akasema;

    “Mama yangu aliwahi kunambia moyo ndio mafanikio. Chochote kianziacho moyoni lazima kifanikiwe kwakuwa kina dhamira na imani ndani yake.”

    “Kweli. Nashukuru sana kukutana na wewe, Amadu. Kila siku unanipa sababu ya kupigania pumzi yangu.”

    Ulsher alimkumbatia Amadu akambusu shavuni. Amadu alitabasamu akashukuru, kisha wakarudi kwenye mkao wao wa hapo awali wa kuegemea kuta ya kibaraza. Amadu alirusha macho yake angani akaendelea kuutizama mwezi.

    “Kila siku usiku nakuona ukiwa umekaa hapa mwenyewe, unatizama anga kabla ya kwenda kulala. Kwanini unapenda kufanya hivyo?” Ulsher aliuliza. Amadu alitabasamu huku akiendelea kutizama mwezi, akasema;

    “Kila ninapotizama mwezi kwa muda, naona uso wa mama yangu. Namuona baba yangu na dada yangu.”

    “Pole, Amadu.”

    “Ahsante.”

    “Naomba nikuache, usingizi umenielemea sasa.”

    “Sawa. Usiku mwema.”http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    “Nawe pia.”

    Ulsher aliondoka akabakia Amadu peke yake. Baada ya kupita dakika tano tangu Amadu awe peke yake, kuna sauti ya mtu akiomba msaada ilivuma ikitokea upande wa magharibi. Amadu alirusha macho pande zake zote pasipo kuona kitu. Alitoka kibarazani akawa anafuatilia sauti aisikiayo, akafika eneo alipokuta mtu akimkaba mwenzake huku akimuamuru atoe kila alicho nacho. Amadu akanyata akimsogelea mkabaji, alimpokaribia alimpiga shina la shingo kwa kutumia ncha ya kiganja chake kama mtu akataye gogo na panga. Mkabaji akalegea na kumuachia mkabwaji. Amadu akamkamata mkabaji shati akampokonya kisu alichokuwa amekibebelea kisha akamruhusu mhanga wa kukabwa aende zake.

    “Nyie ndio mnaoharibu hili jiji na kufanya lisikalike, mnajifanya majogoo ya mjini, sio?” Amadu aliuliza kwa ukali.

    “Hapana, kaka. Ni maisha magumu tu. Hatupendi kufanya hivi.” Mkabaji alieleza huku akiwa ameipinda shingo yake.

    “Umekosa kazi za kufanya mpaka ukabe?”

    “Hapana, ndugu yangu. Mama yangu anaumwa, amelazwa, inatakiwa pesa kubwa afanyiwe upasuaji maji yatolewe kwenye figo yake. Sina chanzo chochote cha kipato kwa sasa. Kazi niliyokuwa naitegemea imekufa, mwekezaji amefunga kiwanda chake na kurudi kwao baada tu ya utawala mpya kuingia. Sina mbele wala nyuma.” Wakati mkabaji anamalizia kusema hayo maneno, machozi yalikuwa yanamtiririka. Amadu aliacha kushika shati la mkabaji akamwambia;

    “Hili unalofanya si suluhisho, linaweza likakuingiza katika matatizo mengine makubwa. Ukikamatwa ukauwawa? … Nenda katafute kazi nyingine umuhudumie mama yako.”

    Mkabaji alishukuru. Aliacha hata na kisu chake kwa Amadu akaondoka zake.













    Kesho yake mida ya saa tisa ya jioni:

















    “Hallo, mheshimiwa raisi!” Sauti ya Kone ilisikika ikitokea ndani ya chumba. Punde mlango ulifunguliwa Kone akatoka chumbani akiwa kavalia bukta fupi na shati jepesi, akawa anaelekea sebuleni huku simu ikiwa sikioni.

    “Ndio muheshimiwa, kuna taarifa nataka kukupatia … Eeeh toka huku Sierra … Kwa taarifa nilizozipata, keshokutwa kutafanyika sherehe kubwa ikulu ya kuupongeza utawala mpya, wageni kadhaa wamealikwa toka nchi mbalimbali kuja kuhudhuria … ndio, mheshimiwa … Ndio, fursa inaweza ikapatikana … Sumu? … Mi nadhani tukitumia mwanamke itakuwa vyema zaidi, huyo mwanamke ndio atamuwekea sumu mfano kwenye kinywaji … Ndio muheshimiwa … Usihofu, mkuu nitalisimamia hilo vyema … sawa, baadae.” Simu ikakata.













    Baadae mida ya saa kumi na moja:















    “Nadhani hii ni fursa nzuri ya kufanya tukio letu.” Amadu aliwaambia wenzake, “Hiyo sherehe ya ikulu itakapokuwa inafanyika nina imani ulinzi hautokuwa vyema maeneo ya benki kuu, wafanyakazi wakubwa watakuwa wamehudhuria kwenye sherehe hiyo, hata ambao watakuwepo watakuwa wametekwa na hilo tukio. Vile vile wananchi wengi watakuwepo videoni na maredioni kusikiliza na kutizama yanayojiri huko ikulu, hii ndio fursa nzuri, mnaonaje?”

    “Kwangu, naona sawa.” Ussein alijibu na kuongezea, “Ila mipango yetu je?”

    “Kuhusu mipango, hakuna shaka. Tayari nimepata ramani yote toka kwa mjomba, inaonyesha kuanzia juu mpaka chini ya jiji, mitaro na njia zake zote za chini. Cha kufanya ni kesho twende na kupitia maeneo hayo ili tuelekezane kwa ufasaha zaidi.” Amadu alifafanua. Wenzake wakaafiki.

    Saa nane ya mchana siku iliyofuata:

    Magari manne makubwa aina ya Scania yaliyobebelea vifaa mbalimbali vya upambaji yalikuwa yametuama mbele ya ikulu. Walikuwepo watu kadhaa wakitoa vifaa ndani ya magari hayo na kuhamishia chini, watu hao walikuwa wamevalia sare zenye maandishi yaliyosomeka ‘The tight black ceremonial masters’: shati jeupe na suruali nyeusi. Walikuwa bize kweli wakitua matambara, vishikio vya taa, maua makubwa, mabango yenye ukubwa wa kati, maspika makubwa, mafagio, makapeti na kadhalika. Baada ya masaa mawili ikulu ikawa imebadilika na kuwa ya kuvutia zaidi. Kitu pekee ambacho kingemfanya mtu atambue kwamba hapo ni ikulu labda ni uwingi wa walinzi waliotapakaa kila hatua wakiwa wamekumbatia bunduki zao kama vile wapo eneo la vita.

    Mwanaume mmoja mrefu aliyekuwa anawasimamia wenzake kupamba na kuremba alimfuata mojawapo ya walinzi akamuambia:

    “Naomba utuitie meneja.”

    Mlinzi akafanya alichoagizwa.

    “Meneja, tayari tumemaliza.”

    Meneja akapekua eneo na macho yake makubwa kisha akaguna.

    “Una uhakika?”

    “Ndio, meneja.”

    Meneja akatupa tena jicho lake kutizama.

    “Sitaki ile rangi ya mapazia uliyopambia pale jukwaani. Nani kakuambia utumie kijani, bluu na nyeupe?”

    “Kwasababu ni rangi ya bendera ya taifa.”

    “We huoni haijapendeza?”

    “Kwahiyo nibadilishe, mkuu?”

    “Aaaahmmm … Embu weka na nyekundu kidogo, nyeusi na nyeupe.”

    “He! … Meneja, hiyo si itakuwa rangi ya MDR?”

    “Kuna shida kwani?”

    Meneja akaondoka. Mpambaji akawarudia wenzake na kuwataka wafanye mabadiliko kwenye mapazia waliyoyatandaza jukwaani. Kazi ikafanyika na kwisha, meneja akaitwa tena kutizama, ngekewa mabadiliko yakampendeza machoni.http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    “Safi sana. Sasa ujira wenu mtaupata.”

    Wapambaji wakaonesha meno yao kwa tabasamu. Meneja akaondoka kwenda ndani. Mlango wa chumba alichokuwemo General ulifunguliwa akaingia meneja akiwa anatabasamu.

    “Kila kitu sasa kipo sawa sasa, mkuu.”

    General akatabasamu na kutengenezea kola ya shati lake la jeshi. Alikuwa ameketi juu ya kitanda kikubwa chenye shuka jeupe kama usufi na mito mikubwa kadhaa. Chumba kilikuwa kikubwa mno na chenye kila mahitaji. Sakafu yake ilikuwa imefunikwa na zulia la manyoya, ukutani kulikuwa kumepachikwa kioo kikubwa chenye fremu rangi ya dhahabu.

    “Safi sana, Thomas.” General akasema, “Kuna cha ziada?”

    “Ndio, kipo, mkuu.”

    “Kipi hiko?”

    “Naomba uniruhusu …”

    Meneja akaufuata mlango akaugonga mara tatu, mlango ukafunguliwa na mlinzi wakaingia wanawake hamsini, wote wakajipanga mstari. Meneja huku akiwa ametabasamu akamtizama General.

    “Haya ni maua yatakayopendezesha shughuli yetu.”

    Alisema Meneja kisha akawatizama wale wanawake na kupandisha kichwa. Wanawake wote wakavua nguo zao na kubakia uchi wa mnyama. General akaonyesha tabasamu. Alinyanyuka akaanza kuwakagua wanawake kwa kuwashika-shika maungo yao. Alipomaliza alimpa mkono Meneja.

    “Safi sana! Hakika hivi viatu vimekutosha.”

    “Nashukuru sana, mkuu.”

    “Shughuli yote hii ipo mikononi mwako.”

    “Bila shaka nitaitendea haki.”

    “Sawa. Waweza kwenda sasa.”

    Meneja na wanawake wake wakatoka nje ya chumba. Meneja akawakusanya wanawake nje ya jengo la ikulu akawaambia:

    “Naomba mhakikishe mnakuwa vema mbele ya wageni. Mnalipwa pesa nzuri na nategemea huduma nzuri kutoka kwenu.”

    Mwanamke mmoja akamjibu Meneja.

    “Hii ndio kazi yetu, hatuna desturi ya kulipua. Tunajua nini cha kufanya bwana Meneja.”

    Siku hazigandi, siku ya tafrija ikatimba. Wakati kukiwa ni jioni muziki laini wenye mahadhi ya kiafrika ukawa unapigwa taratibu. Sauti za wasanii mashuhuri wa bara la Afrika kama Yvone Chakachaka, Kanda Bongoman na Youssour Ndou zilikuwa zinavuma. Watu wa rangi mbalimbali walikuwa wamejazana kwenye uwanja wa ikulu. Kila mtu alikuwa ameshikilia kinywaji chake huku wahudumu wakihakikisha kila ambaye glasi yake imekaukiwa anahudumiwa haraka iwezekanavyo. Hakukuwa na viti, watu wote walikuwa wamesimama. Walinzi walikuwa wametawanyika kila upande wakihakikisha usalama unakuwepo. General Kessy alikuwa akisalimiana na wageni wake mbalimbali wakipeana mikono na wengine wakikumbatiana. Alikuwa tofauti na wengine kwa kuvalia nguo ya jeshi yenye vyeo vya kila rangi kwenye mabega yake na kifuani mwake.







    Baada ya dakika kadhaa za kusalimiana na wageni General Kessy akaenda kwenye kihutubio kilichokuwa kimeketi kwa juu kidogo kiasi cha kuonekana na kila mtu aliyekuwepo lile eneo. Juu ya kihutubio hiko kulikuwepo na kipaza sauti chembamba pamoja na chupa ya maji ya kunywa. General alisafisha koo lake kwanza alafu akaanza kutema maneno:

    “Nashukuru sana kwa uwepo wenu hapa, mabibi na mabwana. Ni faraja kwangu kuona kuna watu ambao bado wanaitakia mema Sierra Leone.”

    Wakati hayo maongezi yanaendelea upande mwingine wa nchi THE GHOSTS walikuwa wanajiandaa kwa ajili ya tukio lao la ukwapuzi wa pesa benki kuu wakivalia nguo za kazi na kupaki vifaa vyao vya kazi mabegini. Nyenzo kama nyundo, vifaa vya utobozi, gloves ngumu, kamba, mtungi wa gesi, kurunzi, ngazi ya kufunga na kufungua, baruti na ramani vilibebwa. Kila mtu alikuwa amevalia kofia nyeusi aina ya boshori pamoja na gambuti. Walijiweka kwenye gari dogo jeusi wakaondoka eneo la nyumbani kwa mwendo wa kawaida usiopalilia mashaka.

    “Nitahakikisha nchi inakuwa salama kwa nguvu zangu zote.” General aliendelea kuhutubia wageni. “Alikunywa maji kidogo alafu akaendelea.

    “Sitokuwa na huruma na wale wote watakaodiriki kwa njia yoyote ile kuhatarisha usalama wa nchi yangu. Nitakuwa rafiki kwa marafiki zangu na adui kwa maadui zangu. Tumeichukua hii nchi kwa lengo la kuifanya isimame tena kwa miguu miwili, na tunaamini itasimama. Hao wazungu wanaonitishia kukata mahusiano na mimi na hata baadhi ya vi-nchi vioga vya Afrika, hainisumbui wala kuninyima usingizi kamwe. Nitakuwa wa kwanza kuonyesha ulimwengu kwamba nchi za Afrika zaweza kujitegemea.”

    Wageni wakapiga makofi kupongeza. Kone akiongozana na mwadada mrembo mwenye shepu ya kujaa wakaingia eneoni. Kone alikuwa amevalia suti ‘taxido’ nyeusi ikiwa imemkaa vizuri mno. Mwanamke aliyeongozana naye alikuwa amevaa gauni refu jekundu la kung’aa, shingo yake nyembamba ilikuwa imebebelea mkufu wa silva ukifanana na bangili yake mkononi.

    Kone alishusha pumzi ndefu akamwambia mwanamke aliyekuja naye.

    “Yule unayemuona pale juu anaongea, ndiye tageti yako. Hakikisha unamtia mkononi na unatimiza adhma. Natumai hautoniangusha. Najua hawezi kuzuia mihemko yake kwa mwanamke mrembo kama wewe.”

    “Nitajitahi kwa akili na nguvu zangu zote.” Mwanamke akajiapiza.

    Umbali wa hatua zisizozidi hamsini toka uzio mkubwa wa benki kuu palikuwepo na mfuniko wa chuma juu ya barabara ya sakafu. THE GHOSTS walisogelea mfuniko huo kwa tahadhari, Amadu akachoropoa nyundo na bisibisi ngumu akaanza kutawanya na kuvunjavunja saruji iliyokuwa imekamata kingo za mfuniko. Alipomaliza alipenyeza bisibisi chini ya mfuniko alafu akapiga na nyundo, mfuniko ukapanda juu, akaudaka na kuuvutia pembeni, likaonekana shimo jeusi lisilojulikana wapi laishia.

    “Hii ndio njia!” Amadu akawaambia wenzake. Akachomoa kurunzi na kumulika ndani pakaonekana mtaro washuka chini lakini mbele bado kukiwa ni giza nene.

    “Una uhakika ndio hapa tulikuja mchana, Amadu?” Ulsher aliuliza. Amadu akatikisa kichwa.

    “Ndio hapa. Tufanye haraka kabla hatujaonekana.”

    Wote wakadumbukia ndani ya shimo na kurudishia mfuniko. Walitua sehemu yenye maji machafu kimo cha magotini, kila mtu alimulika na kurunzi yake wakasonga mbele kama ramani isemavyo. Kulikuwa na mende na panya wa kutosha humo ndani pia joto la makadirio ya nyuzi joto arobaini na tano lililofanya wajae jasho ndani ya muda mfupi tu. Baada ya mwendo wa dakika kama tatu na nusu wakafika sehemu ambapo mtaro wa maji umegawanyika na kutengeneza njia panda. Hapo Amadu akasimama na kunyooshea kidole dari.

    “Ni hapo juu. Inabidi tupasue hapo juu!”

    Farah akatoa ngazi na kuifungua akaibananisha ukutani. Akapanda mpaka juu akaanza kutoboa dari na mashine tobozi. Kwa muda wa dakika, hakuna kilichofanikiwa. Palikuwa pagumu mno kupenyeka.

    “Haiwezekani!” Farah akawaambia wenzake.

    “Tumia njia ya pili.” Amadu akashauri. Farah akapachika baruti kisha akashuka wakasogea kando.

    Puuuuh! Baruti likalipuka na kutawanya ikabakia tabaka jepesi sasa. Farah akapanda tena juu na kifaa tobozi chake akapenyeza chuma mpaka juu. Mtungi wa gesi ukatobolewa na kupenyezwa mrija, mrija ukapitishwa kwenye tundu lililotobolewa kisha gesi ikafunguliwa, taratibu ikaanza kuingia na kusambaa ndani ya benki. Gesi ilipokwisha, mrija ukachomolewa na kupachikwa kwenye mtungi mwingine uliotoka kwenye begi la Ussein, kazi ya kusambaza gesi ikaendelea.

    General alimaliza kuhutubia, wageni wakapiga makofi mazito. Alimiminiwa glasi ya mvinyo akainyanyua juu.

    “Kwa wale wanaoitakia mema Sierra Leone!”

    “Kwa wale wanaoitakia mema Sierra Leone!” Wageni wakaitikia huku wakiwa wamenyanyua vinywaji vyao juu kisha wakavipeleka vinywani.

    Ndani ya benki wafanyakazi walianza kupata mawenge na kupoteza uwezo wa kuona vema. Punde wote walilala, ikiwemo na walinzi wa ndani. THE GHOSTS waliingia ndani ya jengo wakiwa wamefunika nyuso zao na vinyago vya kujikinga na gesi. Wakavunja kamera na zingine kuzipulizia spray. Walichukua funguo za milango toka kwenye kwenye ubao wa ofisi, wakafungua milango kadhaa. Kwenye milango iliyohitaji alama za vidole wakawachukua walinzi na kuwawekesha viganja vyao kwenye kioo. Walipofika kwenye makabati magumu ya kuhifadhia pesa hapo kukaleta kidogo mushkeli.

    “Tutumia baruti?” Mou akauliza.

    “Hapana!” Ulsher akajibu, “Kama tukitumia baruti na hapa, tutazalisha sauti kubwa sana na kudaka mishangao toka pande mbalimbali. Polisi wanaweza kuja muda si mrefu.”

    “Sasa tunafanyeje?” Mou akauliza tena.

    “Nina wazo,” Ulsher akasema. “Inabidi tujue kilipo chumba cha ulinzi, huko kutakuwa na video zote zinazoonyesha kila kamera iliyo humu ndani.”

    “Alafu?” Mou akadakia.

    “Alafu tutatafuta kamera inayotizama hili eneo. Tutarudisha nyuma mkanda na kutizama pale namba za siri zinapoekwa. Tutaivuta picha kwa karibu na kunakili namba hizo.” Ulsher alifafanua. Amadu akamkumbatia kwanguvu.

    “Una akili sana! … Wote tufanye kama Ulsher alivyosema. Tufanye haraka, ndani ya dakika tatu tu.”

    General alishuka kwenye kihutubio akaungana na nyomi la wageni wake. Hiyo ikawa fursa kwa Kone na mrembo wake ambao walijisogeza taratibu mpaka eneo alilopo General, wakamsalimia.

    “Naitwa Kone, mwakilishi wa serikali ya Guinea.”

    General akatabasamu kwa kejeli.

    “Ajabu. Raisi wako ni jirani yangu, ina mana ameshindwa kuja mpaka atume mwakilishi?”

    “Hapana, mheshimiwa, amebanwa na kazi. Ila pia hakuweza kukaa kimya wakati nyumba ya pili kuna tafrija, ndio mana akatuma mwakilishi angalau uwepo wake utambulike.”

    General akatabasamu kisha akamtizama mwanamke wa pembeni.

    “Na huyu ni nani?”http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    “Anaitwa Rose: rafiki yangu wa Sierra Leone.”

    “Ni mpenzi wako?”

    “Hapana, mheshimiwa. Rafiki yangu tu.”

    General akamtizama mwanamke kuanzia juu mpaka chini, aliporudisha macho yake juu akakutana na tabasamu mwanana la mwanamke likishikana na macho legevu.

    “Naweza nikatembea hatua kadhaa na rafiki yako?”

    “Unaweza tu, mheshimiwa. Hakuna tatizo.”

    Mwanamke akapenyeza mkono wake kwenye kwapa la General wakaondoka baada ya kukonyezana na Kone. Walitembea hatua kadhaa huku General akisifu uzuri wa mwanamke aliyeambatana naye. Baada ya kuuliza kama ana mwanaume na mwanamke kujibu hana, General akapenyeza rupia:

    “Naweza nikawa nawe usiku wa leo?”

    Mwanamke akatabasamu.

    “Sidhani kama nitakuwa na muda, mheshimiwa.”

    “Kwanini?”

    “Mimi ni mfanyabiashara, nakuwa bize.”

    “Kwahiyo siwezi kuwa nawe kabisa? … Tafadhali, nitarepea hasara utakayopata kwa kutozingatia biashara yako kwa dakika utakazokuwepo hapa nami.”

    “Kweli?”

    “Unadhani mkuu wa nchi anaweza danganya?”

    Mwanamke akatabasamu tabasamu pana. Wakaongozana na General kwenda ndani ya ikulu. Walipoingia ndani ya chumba, General akaanza kumpapasa na kumtomasa mwanamke kwa pupa. Mwanamke akamsukumizia General kitandani kisha akavua nguo zake zote na kuanza kucheza kwa madaha mbele ya macho ya General yaliyojaa uchu. General alishindwa kuvumilia, alinyanyuka akamfuata mwanamke kwa hamu. Mwanamke akamnong’oneza sikioni:

    “Kalete vinywaji kwanza.”

    Haraka General akafungua mlango na kumuagiza mlinzi alete vinywaji. Vilipoletwa vilipokelewa na Mwanamke akiwa amevalia taulo, General alikuwa yu bafuni anaoga. Huo ukawa upenyo kwa Mwanamke kutia sumu kwenye kinywaji cha General kisha akakichanganya vema. General akatoka bafuni na kumkuta mwanamke uchi wa mnyama, mkononi mwake akiwa kabebelea glasi ya kinywaji.

    “Karibu.”

    General akasogea na kutwaa kinywaji chake. Kabla hajanywa fundo, hodi ikagongwa mlangoni. General akaweka kinywaji chake chini akauendea mlango.

    “Samahani mheshimiwa kuna tatizo limetokea.” Aliongea mlinzi kwa sauti nyenyekevu lakini yenye tahadhari ndani yake. Macho yake yalionyesha hofu kana kwamba anaogopa kusema kilichomleta.

    “Tatizo gani?” General aliuliza hali akitizama tizama usalama na macho yake makavu.

    “Kuna taarifa zimetufikia hivi punde. Benki kuu imevamiwa. Pesa nyingi mno zimeibiwa.”

    Kabla ya kutia neno General akitoa kwanza macho kwa hasira. Alijua fika pesa iliyopo benki kuu ndiyo ambayo anategemea na inampa kiburi. Sasa imekombwa! Alikabwa na kigugumizi.

    “Saa … sa … saa ngapi! Saa ngapi tukio hilo limefanyika? … Umesema ni ndani ya muda mfupi.” Alijijibu mwenyewe.

    “Ndio mheshimiwa.” Mlinzi alijikuta akijibu kwa hofu.

    “Hakikisha mnabana njia zote kuu, asitoke mtu yeyote nje ya jiji. Nataka watuhumiwa wakamatwe ndani ya masaa ishirini na nne na pesa yote irudi! Haraka!” General aliamuru kwa ukali. Uso wake ulieleza jinsi alivyogadhabika. Mlinzi alifungua miguu yake upesi kutoka eneo hilo, kabla hajafika mbali aliitwa na General kwa ukali akageuza shingo yake.

    “Mwambie Talib aje haraka iwezekanavyo!”

    “Sawa mkuu!” Mlinzi aliitikia kisha akatokomea akikimbia kama vile hataki kuitwa tena. General aliingia ndani akavaa nguo zake haraka. Alimtaka na mwanamke avae nguo zake kwani wanaondoka wataonana siku nyingine atakampopigia simu akimuhitaji. Baada ya mwanamke kujibaraguza kimahaba ya uongo kwa General kama vile mtu anayempenda kumbe ana hila nyuma yake, General alimuaga kwa kumpa mabusu motomoto na kusogeza ahadi ya kuonana karibu zaidi. Kwa muda kidogo akasahau matatizo yake mpaka pale alipokutana na Talib uso kwa uso, hapo akawa kifaru aliyejeruhiwa.

    “Talib, umewapata?”

    Aliuliza kama vile ametoa amri mwezi au juma lililopita.

    “Hapana mkuu. Ila nimeshatoa agizo njia zote zibanwe, na makachero wangu wanafuatilia kwa ukaribu mno!”

    General akasonya. “Sitaki hadithi, Talib.” Alifoka, “Nakupa masaa machache tu, niwaone wahusika wote wakiwa kitanzini.”

    “Sawa, mkuu. Nitafanya juu chini. Lakini kwa mujibu wa kamera za nje na za ndani kabla hazijaathiriwa zinaonyesha wahusika ni Amadu pamoja na wenzake aliotoroka nao.”

    Taarifa hiyo ikamgutua Kessy. Ni kama vile alikuwa amewasahau watu hao ambao kwa sasa wanaonekana kumuadhibu. Alikunja ngumi kwanguvu akisaga meno. Macho yake yalikuwa mekundu kana kwamba amekula pilipili. Alipanda gari lake akiongozana na msafara kwenda eneo la tukio – benki kuu. Huko alitazama mazingira yote yaliyoonyesha namna tukio lilivyotekelezwa na kuambiwa kiasi halisi cha pesa kilichokuwa kimeibwa, taslimu dola za kimarekani laki moja, ambayo ni sawa na kiasi cha Leone milioni mia tano sitini nne na laki tano! Kwa namna uchumi wa nchi hiyo ulivyokuwa umeyumba, hiyo pesa ilikuwa kubwa sana. Pesa ilikuwa imefujwa sana na serikali kiasi kama hicho kuibiwa, lilikuwa ni pengo kubwa sana.

    “Talib, nataka hawa watu haraka!” Kessy aliropoka. “Nataka wanyongwe!”

    “Ndio, mkuu!”

    “Nakupa juma moja tu!” Alisisitiza. “Juma moja tu!”

    Usiku huo uligeuka ukawa mchungu mno kwa Kessy. Alilala kitandani kwake mawazo yakimtinda mno ni kwa namna gani atawapata wadhalimu wake na kurejesha pesa yake. Aliamka mara kwa mara akampigia simu Talib akimpa maelezo. Hakutaka kabisa mtu yeyote atoke nje ya jiji la Freetown kwa kutumia njia yoyote ile: angani, majini wala ardhini. Alitaka vyombo vyote vya habari vitangaze jambo hilo na sura za watuhumiwa zikiwekwa wazi huku donge nono la zawadi likiwa limeongezwa maradufu.

    Tofauti na siku zingine, siku hiyo Kessy alikuwa mwenyewe ndani ya chumba chake. Hakuwepo mwanamke yoyote wa ‘kumfariji’, kama vile asemavyo kila uchwao. Tena siku zingine huwa na wanawake zaidi ya wawili japokuwa mara kwa mara wanawake hao huwa wanaishia kupigwa, kuingiliwa kimabavu ama kinyume na maumbile. Yote yakiwa ni kwasababu Kessy hakuzoea raha za kupewa taratibu ama madaha. Kuishi kwake misituni kwa jina la waasi kulimharibu akili kwa namna moja ama nyingine.















    Masaa matano mbele:













    Rose, mwanamke mrembo alikuwa amevalia gauni jekundu lililomkaa vema, alikuwa amekaa na Kone ndani ya mgahawa ulio karibu na bahari. Uso wake ulikuwa umerembwa vizuri na kukupa kila sababu ya wewe kumtazama. Kone yeye alikuwa amevalia suti nyeusi, kama anavyopenda mara nyingi. Ukimwona kwa mwili wake na muonekano basi ungepata kusema ni afisa wa serikali ama mtu mweye nafasi kubwa sehemu nyeti za serikali. Ukiachana na utofauti wao huo, wote walikuwa na utulivu usoni ila pia usiri. Walikuwa wanaongea taratibu wakiwa wamejitenga na umati wa watu. Walikuwa waangalifu na wenye kubeba tahadhari.

    “Kama isingelikuwa hilo jambo la benki, ningelikuwa nishammaliza,” alitamba Rose akiongea kwa pozi. “Tayari kinywaji chake nilishatia sumu. Nilikuwa namngojea anywe tu, kazi iwe imekwisha.”

    Kone alikunywa kwanza juisi yake alafu akatazama baharini.

    “Mungu wake bado kijana,” alisema. “Ila muda wake utawadia tu. Lazima afe kwa namna yoyote ile.”

    “Sasa hivi umepangaje sasa?” Aliuliza Rose akimtazama Kone na macho malegevu.

    “Mpango wetu unategemea na wewe,” Kone alijibu.

    “Kivipi?”

    “Inategemea siku atakayokuita na wapi atakapokuitia,” alieleza Kone. “Kama akikuita uende Ikulu, itakuwa rahisi zaidi. Na sidhani kama kutakuwa kuna njia nyingine nzuri zaidi ya kummaliza na sumu.”

    Kuka kimya kidogo upepo wa bahari ukipuliza.

    “Unajua nataka nikuweke mahala salama,” Kone alisema. “Ukitumia sumu niliyokupa, hatakufa kwa haraka. Inaweza ikamchukua hata siku mbili tofauti na kama ukitumia njia zingine amabazo zitakuweka matatani kiusalama.”

    Rose akatikisa kichwa kuridhia.

    “Ila ni wakina nani hao walioiba benki kuu?” Aliuliza. Alijikuta amepata hamu ya kutaka kujua aliyeharibu mpango wao.

    Kone alisonya akakuna kidevu. Alitazama upande wake wa kushoto, mbali akawaona wanajeshi wawili wakiwa wanabandika makaratasi kwenye kuta za nyumba, mistimu na miti. Alitazama kwa umakini akagundua neno moja kubwa jeusi kwenye tangazo hilo: WANTED. Pasipo kujiuliza mara mbili, Kone akawa amegundua ni wakina nani wanaotafutwa.

    “Adui wa adui yako ni rafiki.” Alisema Kone kisha akamtazama Rose. “Watu walioiba benki kuu ni mojawapo ya watu waliokuwa pamoja na Kessy kwenye kundi lao la waasi kabla hawajapata madaraka.

    “Wapo wangapi?”

    “Watano.”

    “Tu?”

    “Ndio, ila bila shaka umeona madhara yao. Inabidi tuwatafute hao watu. Tukiwapata kazi itakuwa rahisi sana na iliyojaa matumaini.”

    “Utawapataje?”

    “Penye nia pana njia. Nitawapata karibuni kuliko unavyodhani.”

    “Vipi kama ukiwapata nikiwa tayari nimeshamuua Kessy?”

    “Bado itakuwa bora zaidi. Nina matumaini wao ndio watakaimu nafasi ya Kessy. Na kama tutakuwa tumewasaidia kwa njia moja ama nyingine basi tunatumai makubaliano yaliyowekwa kati ya Assessoko na rasi wetu yatatimia.”

    “Naweza nami nikapata nafasi ya kushiriki?”

    “Bila shaka, Rose,” alijibu Kone kisha wakagongesha glasi zao za juisi wakiziambatanisha na tabasamu.





    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Masaa mawili mbele:



    Tayari Amadu na wenzake walikuwa wamemhamishia makazi mama yake Chui kwa kumtafuta nyumba bora zaidi tofauti na pale pa awali. Walimuachia pesa za kujikimu na kisha wao wakatafuta mahala pengine pa kupanga mambo yao wakiwa mkononi na pesa za kutosha.

    Walikuwa ndani ya gari Toyota Landcruiser yenye vioo vyeusi. Walijongea na gari lao hilo mpaka kwenye fukwe ya bahari ya Atlantiki, huko wakaona ndio salama zaidi wakashuka wakipunga upepo huku wakipanga ya kupanga. Ni wapi watapata silaha, alafu mengine yafuate: wapi waanze napo kuijeruhi serikali dhalimu iliyopo madarakani, hayo ndiyo yalikuwa ya kujadili. Kulikuwa ni patulivu na watu kadhaa wakiwa wanaoga kwenye maji ya bahari walikuwa wanaonekana mbali na uwepo wa THE GHOSTS. Hakukuwa na kitu cha kuhofia kwa muda huo.

    “Ni Liberia pekee ndipo tutapata bunduki kwa urahisi,” alishauri Mou. Vita kati ya kundi la waasi la Le tueurs na serikali ya Liberia ambayo ilikuwa inapumulia mashine kwa sasa, ilimfanya Mou aamini silaha zitapatikana huko kwa wepesi. Kutokana na mahusiano waliyokuwa nayo kati ya wao na Le tueurs, basi watapata kile wanachokitaka haswa ukitazamia wana pesa za kutosha. Ila Amadu akatilia hilo jambo walakini:

    “Sidhani kama itakuwa rahisi kiasi hiko,” alifungua kauli. “Hakuna anayejua kama Kessy atakuwa ameshawasiliana na hilo kundi juu yetu. Kwenda huko ni hatari zaidi, wanaweza wakatushambulia badala ya kutusadia.”

    Ilikuwa ni vema kuchukua tahadhari, na Amadu alikuwa mwepesi mno kwenye hilo.

    “Kundi la Le tueurs wanajuana na Kessy. Unakumbuka ile barua niliyokabidhiwa na yule mtu wao kwenda kwa Kessy? – ile barua ya siri? – kwanini ilikuwa ya siri. Kessy hakuwahi kumuonyesha Assessoko maudhui ya ile barua na mwishowe alimuua pia. Kundi la Le tueurs na Kessy wanajuana, na dhamira zao ni moja.”

    Maelezo hayo yalimridhisha kila mtu lakini pia yalifungua uwanja mpana zaidi wa kuendelea kujadili ili wapate jibu. Ni wazi hawawezi wakafanya lolote kama wasipokuwa na silaha. Hata kipindi MDR inatafuta madaraka, wadhamini toka nje pamoja pia na majirani walihusika kwa namna moja kuwasambazia silaha za kukamilisha malengo yao.

    “Tukavamie kambi ya jeshi.” Alishauri Ulsher. Wanaume wote wakamtazama. Ni kama vile ahwakutegemea kwa shauri kama hlo kutoka kwenye kinywa cha mwanamke.

    “Kwanini umeona hilo ni sahihi?” Aliuliza Ussein.

    “Kama malengo yetu ni kuidhoofisha na kuiondoa serikali,” alianza kuelezea Ulsher. “basi kuishambulia kambi ya jeshi itakuwa njia nzuri sana ya kurahisisha hilo zoezi. Kwa pamoja tukifanya hivyo, tutakuwa tumepoka silaha zao, tumepunguza wapambanaji wao, na kitawagharimu fedha pia.”

    “Ni kweli, ila linahitaji uangalifu sana.” Alitahadharisha Farah.

    “Kila tunachofanya kinahitaji uangalifu sana.” Alisisitiza Amadu. “Kuvamia kambi ya jeshi, haswa kipindi hiki ambacho si muda mrefu tumevamia benki, lahitaji uangalifu wa hali ya juu.”

    Wenzake walimuunga mkono. Ni kweli lilikuwa na hatari kubwa, ila lazima walitakiwa walifanye hilo kama kweli wamelenga kupindua nchi. Na kufanya hivyo maana yake kunahitaji mipango, hivyo wakaridhia kwanza kutembea eneo hilo kabla hawajafanya lolote. Kazi hiyo alipewa Farah na Mou. Na tena ilitakiwa itekelezwe usiku wa siku hiyo!



    Masaa saba mbele:



    Gari la THE GHOSTS, Toyota Landcruiser lilisimama umbali wa kilomita tano tokea ilipo kambi ya jeshi ya Murray Town Barracks. Halikuwa limewashwa taa na lilikuwa likitembea taratibu mno mpaka hapo penye kificho cha miti lilipokomea. Dereva Mou alitumia tu macho yake na mwanga wa mwezi kuliongoza gari. Yeye pamoja na Farah walishuka toka kwenye gari hilo, wakashika njia kufuata kambi. Walitembea kwa tahadhari wakihakikisha hawasikiki wala kuonekana. Kila mtu alikuwa na bunduki ndogo ameishikilia mkononi.

    Baada ya kutembea kama mwendo wa kilomita moja, walianza kusikia sauti za watu na vishughuli vya hapa na pale. Walizidi kujongea karibu zaidi, na hivyo sauti zikawa zinazidi kuwa kubwa. Walifika mahali penye ukuta mkubwa mrefu uliokuwa unafumba kambi hiyo, juu ya ukuta huo kulikuwa kuna vyupa vikiwa vimesimamishwa dede. Hapo sasa ikabidi mbadala ufanyike kwani ilikuwa lazima waingie humo ndani wapate kusoma ramani.

    Mou aliinama, Farah akakanyaga mgongo wa mwanaume huyo, akasimama kuchungulia ndani.

    “Hapa si pazuri. Twende upande wa kusini!” Alisema Farah. Aliona hatari zaidi kuingilia pale kwani ndani yake umbali mfupi walikuwapo wanaume waliovalia gwanda za jeshi wakiwa wamebebelea bunduki ‘SMG’. Walifika upande huo wa kusini wakarudia mtindo walioufanya hapo awali. Farah alipanda na kuvunja vyupa kabla hajakwea ukuta na kumvuta mwenzake kuzama ndani.

    Lengo kubwa lilikuwa ni kujua mahala lilipo ghala la silaha, eneo analokaa mkuu wa kambi na hadhi ya usalama.

    Ndani ya dakika nane katika kambi hiyo, Mou na Farah walitimiza yote hayo. Kazi ilibakia kwenye kutoka ndani ya kambi hiyo ambayo iliwalazimu mara kwa mara kujificha kukwepa wanadoria na taa kubwa iliyokuwa mnarani ikizunguka muda wote kwenda kulia, kushoto, kati na juu.

    Waliufikia ukuta Farah sasa hivi akakamata ukuta wakati Mou akikwea mgongo wake na kumvuta mwenzake kutoka nje. Walitua na kuondoka eneo hilo upesi kufuata gari lao. Walifika wakamkuta mwanajeshi mmoja akiwa hapo na mbwa wake. Alikuwa amefika muda si mrefu na bado hakuwa ametoa taarifa yoyote kwa wenzake.

    Sasa ilibidi Farah na Mou wafanye upesi. Si tu kwamba wawahi taarifa kabla haijatolewa, bali pia wawahi kabla pua ya mbwa haijatia nongwa. Walijigawa haraka kwa ukimya kwenda pande tofauti. Baada ya muda mfupi tu, mbwa akaanza kubweka upande alipo Farah. Mwanajeshi alitazama pande hiyo akiinyoshea mdomo wa bunduki. Ghafla akajikuta akisulubiwa na teke kali toka kwa Mou aliyetokea nyuma. Farah naye alichomoza akadaka bunduki ya mwanajeshi huyo kisha amkakandikia nayo mbwa kwa kutumia kitako, mbwa akazirai.

    “Amekufa?” Farah aliuliza wakimtazama mwanajeshi aliyekuwa amelala akiachama mdomo. Mou aliweka mgongo wa kiganja chake kifuani mwa mwanajeshi huyo kisha akabinua mdomo wake.

    “Sis’kii mapigo ya moyo.”

    “Sasa tunafanyaje?”

    “Itabidi tumchukue.” Mou alishauri. “Kama tukimuacha hapa, ataonekana mapema na kusababisha tensheni kubwa kambini. Inaweza ikawa tatizo.”

    Wasipoteze muda zaidi, walimchukua mwanajeshi huyo na mbwa wake wakayoyoma toka eneo hilo. Walitembea umbali wa kilomita kama tano ama sita, wakamtua mwanajeshi yule kumtupia huko. Walimbeba mbwa tu waliyefika naye mpaka mahali pa siri wanapoishi.

    Wakaeleza yale yote waliyopata kuyaona.



    Masaa sita baadae: Ikulu ya Guinea.



    “Haloo!” Raisi alizungumza. Alikuwa amevalia kanzu ndefu nyeupe pamoja na kofia yake. Alikuwa ameketi mezani alipokuwa anakunywa chai kufukuza kabaridi cha asubuhi. Alipomaliza tu kunywa chai hiyo, hakuwa na subira, akampigia simu Kone kuulizia ni wapi alipofikia kwenye mchakato wake wa kumtia adabu Kessy aliyekiuka makubaliano aliyoyatia na marehemu Assessoko.

    “Mbona kimya, Kone?” Raisi aliuliza. Uso wake ulikuwa mkavu na alikuwa ana hamu na majibu. Bahati mbaya kwake, majibu ya Kone hayakumkuna. Bado Kessy alikuwa hai akiokolewa na tukio la benki kuu kukombwa.

    “Sasa inakuaje Kone?”

    Kone akamuelezea raisi wake huyo yale aliyoyapanga na Rose, lakini pia juhudi zake za kuwatafuta Amadu na wenzake ili wasaidiane kutimiza adhma.

    “Sawa, nimekuelewa. Ila pia kuna jambo ningependa kukushirikisha,” alisema Raisi kisha akavuta pumzi. “Jambo hili ni nyeti na kubwa, Kone. Nisingependa kuliongelea simuni. Panda ndege uje Guinea sasa hivi.”

    Kone alitii agizo la raisi wake, alikata tiketi upesi aende Guinea. Kwenye uwanja wa ndege kulikuwa kuna ukaguzi mkubwa sana huku picha za wakina Amadu zikiwa zimebandikwa kila hapa na pale. Ila mwishowe baada ya ukaguzi mwingi, Kone alipanda ndege na baada tu ya muda usiozidi masaa matano akawa amefika Guinea, ikulu, kuonana na Raisi.

    Mke wa Raisi aliwapa faragha, wakiwa wamekaa kwenye kibaraza wakiwatazama wanajeshi wanaozungukazunguka na bunduki zao, Raisi alisafisha koo lake akasema:

    “Kone kuna jambo limenifikia mezani jana jioni. Mpaka sasa nimekosa kujua ni uamuzi upi niufanye?”http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    “Ni kuhusu Guinea ama Sierra?” Kone aliuliza.

    “Ni kuhusu Sierra!” Akajibu Raisi. Hapo Kone akavutiwa zaidi. Ni kipi hicho Raisi wake alichomtolea Sierra na kumuitia pale haraka vile? Ni kipi hicho tena Raisi wake anachakusema kuhusu Sierra na si nchi yake, Guinea?



    Moyo wake ulianza tu kwenda mbio. Hakujua kwanini.





    MWISHO WA MSIMU WA KWANZA



    ENDELEA KUFUATILIA MSIMU WA PILI



    MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Blog