Search This Blog

Sunday 20 November 2022

VIPEPEO WEUSI: FROM ZURICH WITH RULES - 3

 





    Simulizi : Vipepeo Weusi: From Zurich With Rules

    Sehemu Ya Tatu (3)







    Kwa kasi na kwa utemi, walinitutusa mpaka ndani ya gari na kisha kufunga milango. Gari lilipokuja lilitokea upande wa kusini na baada ya kunipakia kwa utemi ndani yake waliliondoa kwa kasi kubwa kuelekea upande wa kaskazini.



    Waliendesha umbali mfupi kama dakika tano hivi na kisha kukunja kulia. Kichwani nilikumbuka kabisa hii ndio ilikuwa ile barabara ambayo inamichepuko kadhaa ukikunja kona lakini kama ukibakia kundesha kwa barabara hii kuu uliyochepukia basi inakurejesha tena Hardstrasse. Waliendesha gari kwa kasi bila kuchepuka mahakokote pale na kama baada ya dakika tano hivi dereva alikunja tena kona.



    Nilitabasamu japokuwa nilikuwa nimefunikwa na hili lifuko jeusi la kitambaa, walikuwa wanajaribu kunichanganya akili nisielewe kule ambako wananipeleka lakini walikuwa wamechelewa na niliwazidi akili kabla.



    Gari ilipokunja kona tulielekea kaskazini kwa muda wa karibia dakika kumi na tano nzima. Nilikuwa na uhakika kabisa kuwa tulipita daraja la ule mto mkubwa niliouona kwenye ‘Google Maps’ na muda huu tulokuwa tumeingia eneo la Wipkingen.



    Baada ya kama dakika tano nyingine dereva alikunja kushoto na kisha akakunja kulia na gari likasimama. Nilishushwa mzobe mzobe kwa kututuswa kwa utemi kama ambavyo nilipandishwa. Upande huu wa mji ulikuwa na baridi kubwa tofauti kabisa na upande ule wa mji ambao nilikuwa awali. Nilihisi tumeingia kwenye jengo kutokana na milango mizito ambayo nilihisi ya chuma niliyokuwa naisikia ikifunguliwa.



    Japokuwa nilikuwa sioni mbele lakini nilipokanyaga tu mguu wangu ndani ya jengo hili kitu cha kwanza nilichokihisi ilikuwa ni harufu ya damu. Na sio damu tu bali ni damu mbichi kabisa.



    Mwili wote nilihisi umekufa ganzi ghafla. Japo nilikuwa najiamini kuwa siwezi kuuwawa kabla ya kuambiwa siri niliyokuja kuifukua huku, lakini harufu hii ya damu ilinifanya kujiamini kwangu kuanze kuyeyuka.







    Harufu ya damu ambayo nilikuwa naisikia ilikuwa ni mbichi kiasi kwamba mpaka ilikuwa inachefua rohoni. Nilihisi kwamba eneo hili tuliloingia lilikuwa na ‘hall’ kubwa kutokana na kuakisiwa kwa sauti ya hatua ambazo tulikuwa tunakanyaga sakafuni. Kuna muda nilikuwa nikikanyaga chini nasikia kabisa kwenye kiatu kwamba nimekanyaga kwenye dimbwi la kimiminika. Moyoni nilikuwa naomba iwe ni dimbwi la maji ambalo nilikuwa nakanyaga na si dimbwi la damu.



    Tulitembea kama hatua thelathini hivi au arobaini nikasikia mlango mwingine unafunguliwa. Tulipoingia tu ile harufu ya damu ikakoma. Nilikuwa najitahidi kutumia hisia zangu kwa kadiri nilivyoweza ili kujua mazingira na kile ambacho kilikuwa kinaendelea. Lile fuko jeusi la kitambaa ambalo niliveshwa kichwani lilikuwa linanifanya nishindwe kabisa kupumua sawia na lilinifanya nisikie joto la haja.





    Mikono yangu haikuwa imefungwa kamba kabisa bali mmoja wa wale watu alikuwa ameikunja na kuishikilia kwa nyuma. Kichwani kila aina ya video ya watu kuchinjwa ambayo nilikuwa nimewahi kuiona mitandaoni ilikuwa inanijia. Kwa hakika nilihisi ni namna gani ambavyo dakika zao za mwisho kabla ya vichwa vyao kutenganishwa na viwili viwili zinavyokuwa.



    Tulitembea kama hatua ishirini hivi pale ambalo nilikuwa nahisi kwamba ni korido, kisha nikasikia mlango upande wangu wa kulia ukifunguliwa. Hatukuingia moja kwa moja ndani baada ya mlango kufunguliwa. Nilisikia kama watu wawili ambao tulikuwa nao waliingia kwanza huku mimi na mwenzao au wenzao wengine tukisubiri nje. Tulisubiri kama muda wa dakika mbili hivi kisha nikasikia mlango ukifunguliwa tena kisha tukaingia ndani.



    Baada ya kuingia ndani niliongozwa mpaka upande mmoja wa chumba kisha nikaketishwa kwenye kiti. Lile fuko la tambala jeusi usoni likaondolewa.



    Nikafikicha macho kutokana na kuuma kwasababu ya kukaa gizani kwenye lile fuko jeusi la kitambaa kwa karibia nusu saa nzima. Baada ya kufikicha macho ndipo nikayaangaza mbele yangu.



    Tulikuwa kwenye chumba ambacho kwa kila namna kilionekana kabisa kilikuwa ni chumba cha hoteli. Na hakikuwa chumba cha hoteli ya kichovu, kilionekana ni chumba cha hoteli yenye hadhi fulani ya katikati. Hapa tulipokuwa ilikuwa ni sebule ya chumba hiki. Kulikuwa na masofa mawili upande wangu wa kushoto ambayo yana meza ndogo ya kioo mbele yao. Mimi nilikuwa nimeketishwa kwenye kiti kimoja wapo ambacho kilikuwa ni kiti cha meza ya chakula ambayo nilipogeuka niliona iko nyuma yangu.



    Upande wangu wa kulia kulikuwa na meza ya ukubwa wa wastani ya kiofisi pamoja na kiti chake ambayo juu yake ilikuwa na makabrasha kadhaa pamoja na nyaraka zilizotawanywa tawanywa kuashiria kuwa kulikuwa na mtu muda si mrefu kabla hatujawasili alikuwa kuna kazi anaifanya kwenye meza hii.



    Kwenye zile sofa upande wangu wa kushoto walikuwa wameketi majamaa wawili wa kizungu wote wamenyoa upara na wamevaa majaketi meusi ya ngozi.



    Mlangoni pia alisimama mwingine, huyu alikuwa na ngozi nyeusi lakini naye kama wenzake alikuwa na upara pia amevaa jaketi jeusi la ngozi. Pia nyuma yangu kwenye meza ndogo ya chakula alikuwa ameketi mwingine wa nne. Huyu alikuwa mzungu… lakini naye vile vile pia alikuwa na upara na amevalia jaketi jeusi la ngozi.



    Kwa kuwasoma haraka haraka tu, niligundua kwamba hawa walikuwa ni wale ambao walikuwa wamenitoa kule barabarani na kunileta hapa. Hata namna ambavyo walikuwa wamekaa na kunitazama ilionyesha dhahiri kwamba kuna mtu ambaye walikuwa wanamsubiri na nilikuwa na hakika kabisa mtu huyo alikuwa kwenye kile chumba cha kulala.



    Nilijikuta akili yangu inawaza kuhusu ile harufu ya damu ambayo nimeisikia pale kwenye ‘hall’ kabla ya kuletwa hapa. Kama ingelitokea kwa namna fulani nimeamka ghafla tu ndani ya chumba hiki, moja kwa moja akili yangu ingeniambia kuwa niko kwenye chumba cha hoteli ya kifahari na kwa hakika ndivyo ambavyo hapa tulipo kulivyokuwa kunaonekana. Lakini swali ambalo nilikuwa najiuliza kichwani na lilikuwa likinitatiza ni namna gani au sababu gani hoteli itapakae harufu ya damu mbichi. Na kama ni hoteli wamewezaje kuniingiza wakiwa wamenivesha jifuko jeusi la kitambaa kichwani?



    Majibu yote ambayo yalikuwa yanakuja kichwani yaliniambia kwamba hii haikuwa hoteli. Hili ndilo lilikuwa jibu lenye mantiki zaidi. Lakini wakati kichwani nikipata jibu hili ambalo ndilo hasa lina mantiki, mbele yangu macho yalikuwa yanaona mandhari ya chumba yenye kushawishi kwa asilimia zote kwamba hiki ni chumba cha hoteli.



    Nikiwa bado naendelea kushangaa mandhari ya chumba hiki huku nikikinzana mwenyewe kichwani mwangu kupata tafsiri ya hapa nilipo, ghafla mlango wa chumba cha kulala ulifunguliwa na kutoka mwanaume mzee wa kizungu wa makamo hivi. Kwa makadirio ya haraka nilihisi atakuwa na kama miaka sitini hivi au labda sitini na mbili. Japokuwa hakuwa mzee sana lakini kichwani mwake zote zilikuwa nyeupe na alikuwa amezichana vyema kabisa nywele zake hizo za singa singa.



    Alikuwa amevalia suti nadhifu yenye kuonekana ya gharama kubwa ya rangi ya kijivu ambayo ilishika vyema mwili wake ambao ulionekana kuwa ni wa mazoezi au labda huko nyuma alizoea sana kufanya mazoezi. Mdomoni alikuwa na kipisi cha masigara makubwa kwa umbo ambayo nimezoea kusikia yakiitwa ‘cigar’.



    “Jambo Rweyemamu.!” Mzee alijitahidi kunisalimu kwa kiswahili kibovu kwa lafudhi nzito ya kifaransa.



    Mara moja akili yangu iliweza kukumbuka sauti yake. Japokuwa ilikuwa na tofauti kidogo kuisikia kwa masikio uso kwa uso, lakini sauti hii ndiyo yenyewe hakika kabisa ambayo niliongea nayo kwenye simu nikiwa nyumbani Morogoro na kunipa maelezo ya kuja Zurich. Sauti hii ndiyo ambayo mapema usiku wa leo, au jana kwa usahihi zaidi ambayo ilinieleza kwenye simu nikiwa hotelini kwamba niende kwenye ile hoteli ya kichina. Na ni sauti hii pia ambayo ilinipigia simu muda mchache uliopita nikiwa kwenye lile jengo mtaa wa hardstrasse na kunieleza kuwa watakuja kunichukua ndani ya nusu saa. Huyu ndiye mtu ambaye kichwani mwangu nilikuwa namtamhua kama ‘Hudini’!





    “Hudini?” Nikaongea kwa kuuliza bila kuitikia salamu yake.



    “Hahah do you even know what that means?” Akaniuliza.



    “Its you, right? The one I have been talking to on the phone all this time… its you!” Nikaongea kwa msisituzo mkubwa nikiwa na uhakika kabisa na nilichokuwa nakisema.



    “Let’s get down to business, shall we?” Akaongea huku anaenda kuketi kwenye kiti kilichopo kwenye ile meza ya ukubwa wa wastani ya kiofisi na akakigeuza kiti upande wangu ili tutazamane sawia.





    Alipogeuka kunitazama, tuliganda tukiwa tunaangaliana kwa taribani dakika nzima bila yeyote kati yetu kusema neno lolote lile.

    Tuliangaliana mpaka nikamuona anaanza kutabasamu.



    “What?” Nikamuuliza.



    “Nothing… I just can’t believe it that you are the one who took down one the most powerful organisation in Africa!” Akaongea huku bado akiwa anatabasamu.



    “I didn’t take down nothing… I just did what I had to do for my sake..!”



    “No no no! For Cheupe… hahah is that what you call her? Cheupe right?” Akaongea huku safari hii akitabasamu kifedhuli.



    Sikupenda muelekeo wa mazungumzo yalikokuwa yanakwenda.



    “I thought you said we should get down to business?” Nikamkazia macho.



    “Sure… here I am! Let’s get down to it..”



    Akakohoa kidogo na kuzima lile lisigara likubwa na kuliweka pembeni kwenye kisahani fulani juu ya meza.

    Akafungua droo ya meza kisha akatoa makabrasha kadhaa na nyaraka nyingi na kuziweka juu ya meza.



    Akaanza kupekua pekua na kisha akachomoa kama nyaraka mbili hivi kutoka kwenye ule msitu wa zile nyaraka alizoIweka mezani. Akazishikilia mkononi na kuniangalia huku akijiandaa kuanza kuongea.



    “I believe you know why you are here..!” Akaongea safari hii akiwa ‘serious’ haswa bila tabasamu la utani wala ufedhili.



    “Honestly I don’t know why I am… its my curiosity that brought me here… but I don’t know exactly why am here!” Nikaongea kwa mtindo ule ule nikimuangalia nikiwa serious bila tabasamu wala kupepesa macho.



    “I could assume why your father didn’t want to tell you exactly why you should come here… you wouldn’t have accepted it!! He wanted you to come here to see for yourself and decide!”



    “I am listening!”



    “You are ‘The Replacement’!” Akanijibu kwa kifupi tu huku amenikazima macho.



    “Replacement for what?” Nikauliza kwa shauku.



    Hakunijibu kitu. Akachukua nyaraka moja ambayo alikuwa ameishikilia mkononi na kunikabidhi.



    Ilikuwa ni picha. Picha ambayo imepigwa na kutolewa kwenye karatasi kubwa ya A4. Picha ya ‘black and white’.



    Picha hii iliwaonyesha watu watatu wakiwa wameketi nje ya nyumba. Watu wazima wawili na mmoja mtoto msichana. Yule mtu mzima mmoja alikuwa ni mzungu wa makadirio ya umri wa kama miaka thelathini hivi. Alikuwa amevalia sati yake nadhifu na tai. Mtu mzima wa pili alikuwa ni mtu mweusi. Mwanaume wa umri wa kama katikati ya thelathini, labda thelathini na tano au sita hivi. Mwanaume huyu alikuwa amembeba yule mtoto wa kike kwa kumpakata pajani. Mtoto huyu wa kike alikuwa wa kama miaka mitano hivi au sita.



    Nilihisi moyo unataka kutoka ndani ya kifua kutokana na mapigo ya moyo kwenda kasi mno kwa ghafla. Mtoto huyu wa kike nilikuwa namfahamu kama ambavyo nilikuwa nafahamu kiganja cha mkono wangu. Alikuwa ni Cheupe wangu enzi za utoto wake na huyu aliyempakata alikuwa ni baba yake. Lakini kilichonishitua zaidi sio Cheupe na baba yake bali ni huyu mzungu ambaye alikuwa amekakaa pembeni yao. Sikujua ni kwa nini niliogopa na kushituka moyoni, lakini kwa hakika kabisa kichwani mwangu niliamini kwamba hii haikuwa mara yangu ya kwanza kumuona mzungu huyo na kunahisia mbaya ilikuwa inanijia kila ambavyo niliendelea kujiaminisha kuwa sio mara ya kwanza kumuona mzungu huyo.



    Kana kwamba huyu mzee alikuwa ananisoma akili yangu namna nilivyokuwa nahangaika kukumbuka nimemuona wapi huyu mzungu, bila kunisemesha chochote alinikabidhi nyaraka nyingine ambayo ilikuwa imesalia mkononi mwake.



    Nayo ilikuwa ni Picha nyingine ya ‘black and white’ ambayo imetolewa kwenye karatasi ya A4. Ilibakia kidogo nidondoke chini na kuzimia.



    Picha hii ilikuwa inafanana kabisa na Picha ambayo niliikuta kwenye bahasha ambayo nilikabidhiwa na baba yangu, bahasha ambayo niliifungua siku ile usiku wa manane nilipogombana na Cheupe. Siku ambayo ndio ilizaa mfululizo wa matukio mpaka kunifanya nifike hapa leo hii.

    Picha hii ilikuwa inainyesha watu wanne wakiwa eneo la kama bandari hivi muda wa usiku, katikati ya makontena. Watu wawili kati ya wale wanne wakionekana kama ni walinzi. Mmoja akionekana dhahiri ni Rais Albert Kafumu, Rais wa Jamuhuri Ya Muungano wa Tanzania. Na alikuwa naongea na mtu fulani, Mzungu. Mzungu huyo wa kwenye Picha ya Rais Albert Kafumu ndiye Mzungu yule yule ambaye yuko kwenye Picha ya Cheupe na baba yake. Tofauti pekee Picha ile aliyemo pamoja na Cheupe na baba yake ilipigwa zamani mno. Labda miaka hata ishirini na tano iliyopita. Lakini hii ambayo amepiga na Rais wa Tanzania ilionekana ni ya hivi karibuni, labda mwaka au miaka miwili tu iliyopita.



    Jasho lilinitoka ghafla. Sikujua ni kwa nini au naogopa nini. Lakini jasho lilinitoka na presha ilinipanda.



    “Ray! Now let’s get down to business… and let’s start from the beginning..!” Mzee aliongea kwa kujiamini huku anachukua nyaraka nyingine mezani.



    Nilibaki nimeganda namtazama kama sanamu. Nilihisi mwili wote kama umepooza.





    Kiza kinene. Hicho ndicho kitu pekee ambacho nilikuwa nakikumbuka. Kiza kinene. Kiza kinene na baridi kali hasa maeneo ya tumboni pamoja na woga wa aina ambao ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kuusikia ndani ya nafsi yangu. Maumivu ambayo nilikuwa nayasikia sikuwa nayaogopa kama ambavyo nilikuwa naogopa kila nikitazama damu mkononi mwangu. Sikuwahi kujua hapo kabla ni namna gani mtu anajisikia au anaona pale ambapo anakaribia kifo. Sikiwahi kujua namna ambavyo macho yanaanza kupoteza nuru na kitu pekee ambacho unakiona mbele yako ni kiza. Sikuwahi kujua ni namna gani mwili wako unaweza kuwa na siha njema lakini ukashindwa kuinua hata kidole na kukisogeza.



    Nikarejesha tena mkono tumboni kuzuia damu zisiendelee kutoka. Nikalaza tena kichwa changu sakafuni na kutazama juu angani.



    “Huu hauwezi kuwa mwisho wangu.!!”



    Nilitamka tena kauli ile ile ambayo nilikuwa nairudia tena na tena tangu nimedondoka. Nikainua tena mkono kutoka tumboni na kuutazama namna ambavyo ulikuwa umeloa damu. Macho yalikuwa yameanza kulegea tena kuashiria kuwa naweza kupoteza tena fahamu au labda ndio ikawa safari yangu ya mwisho nisiyafumbue tena.



    Sikuwahi kudhania kabla ni namna gani mtu anajisikia akikaribia kifo. Kwa miaka yangu yote duniani kila nikifikiria kifo kitu pekee ambacho kilikuwa kikinijia akilini ni maumivu. Maumivu makali. Lakini ukweli ni kwamba ukikikaribia kifo hakuna maumivu yoyote ambayo unayasikia. Uhalisia ni kwamba nilikuwa sisikii hisia yoyoye ndani yangu zaidi ya woga. Ndio, woga sio maumivu. Woga wa kufumba macho kwa mara ya mwisho nisiweze kuyafumbua tena. Woga wa kulala usingizi ambao sitaweza kuamka tena. Woga wa kutohisi chochote tena, woga wa kutosikia chochote tena. Licha ya risasi ambayo ilikuwa tumboni mwangu lakini sikusikia maumivu yoyote kadiri mwili wangu ulivyoishiwa nguvu, kadiri macho yangu yalivyozidi kupoteza nuru, hakuna cuembe ya maumivu ambayo nilikuwa naisikia. Kitu pekee ambacho nilikuwa nakihisi kwenye nafsi kilikuwa ni woga.http://pseudepigraphas.blogspot.com/



    Niliangalia mkono wangu namna ulivyojaa damu kisha nikaurejesha tena tumboni.



    Nikajikuta natabasamu. Japokuwa nilikuwa natabasamu lakini kona za macho yangu machozi yalikuwa yanatiririka. Kwa kuwa nilikuwa nimejilaza chali sakafuni, niliyasikia machozi yakitiririka na kuingia masikioni.

    Nilikuwa naogopa kufumba macho kwa mara ya mwisho, lakini nilichokuwa nakiogopa zaidi ilikuwa ni kuondoa kwa namna hii, mahali hapa ambapo naweza kuoza kama mzoga kwa wiki kadhaa bila mtu yeyote kujua.



    Nikajikuta naanza kutathimini na kujitathimini mimi mwenyewe na chaguzi zote nilizozifanya katika maisha yangu. Nikajikuta natamani kama ningepata nafasi nyingine nirekebishe baadhi ya mambo au labda nipate fursa ya kuyafanya tofauti.

    Nikakumbuka namna ambavyo wiki yangu ya mwisho nilivyokuwa nyumbani Tanzania kabla ya kusafiri kuja Zurich namna ambavyo tuligombana na mkewangu Cheupe. Nikakumbuka hasira ambayo nilikuwa nayo kutokana na kumuona kama vile anaondoka kutoka mikononi mwangu kwa kung’ang’ana kwenda Nairobi kufanya kazi.



    Japokuwa uamuzi wangu wa kuja Zurich ulikuwa ni kutokana na kiu ambayo ilikuwa ndani yangu kutamani kujua na kung’amua fumbo ambalo baba yangu alikuwa amenipa kutokana na ile bahasha ambayo aliniachia, lakini pia safari yangu hii ya Zurich pia ilichangiwa na kutamani kupata walau wiki chache kuwa mbali na Cheupe. Uhusiano wetu, ndoa yetu haiko sawa kabisa. Nilijua bila shaka kabisa kwamba ndoa yangu na Cheupe inapitia katika kipindi kigumu na labda Cheupe inawezekana kuna mambo amebadilika tofauti kabisa na Cheupe ambaye nilimpenda kutoka utotoni, tofauti kabisa na Cheupe tuliyepambana kuidondosha jumuiya ya The Bold, lakini kitu kimoja ambacho kamwe hakikubadilika ni kiwango changu cha kumpenda.



    Hakuna jambo linaloumiza moyo kama kushuhudia ukiwa unampoteza mtu unayempenda kutoka mikononi mwako. Akilini mwangu wiki kadhaa zilizopita nilijiapiza kuwa ni vyema niende Zurich kukonga kiu ya kung’amua fumbo nililoachiwa na marehemu baba yangu kuliko kuendelea kukaa nyumbani nikishuhidia mapenzi yangu na Cheupe yakizama siku baada ya siku.

    Lakini muda huu ambao nilikuwa sina hakika kama nitaweza kufikisha hata masaa matatu mbele, hakuna kitu ambacho nilikuwa nakitamani kama kumuona Cheupe akiwa pembeni yangu. Hakuna ambacho nilikuwa natamani muda huu kama nitafumba macho kwa mara yangu ya mwisho basi niyafumbe nikiwa mikononi mwa Cheupe, nipate fursa tena kumueleza jambo moja tu. Moja tu… kwamba nampenda kuliko kitu chochote kile.



    Nilitabasamu tena na kuinua mkono kutoka tumboni na kuungalia jinsi ulivyofunikwa na damu. Nikatabasamu. Kila ambavyo nilitabasamu ndivyo ambavyo mchozi nao ulitiririka kutoka kwenye kona za macho na kudondokea masikioni. Ilikuwa kana kwamba najifariji na hiki kitendo cha kuutoa mkono tumboni na kuungalia mara kwa mara labda kungeweza kusaidia kufanya damu tumboni isiendelee kutoka. Lakini kila ambapo niliinua mkono kutoka tumboni na kuungalia ndivyo woga ndani yangu ulizidi maradufu. Woga wa kufumba macho kwa mara ya mwisho na nisipate nafasi ya kuyafumbua tena.



    Nikaanza kufikiria siku mbili zilizopita. Siku ambayo nilipelekwa mtaa wa Wipkingen hapa hapa Zurich. Siku ambayo nilizibwa sura kwa tambara jeusi la kitambaa ili nisione. Siku ambayo nilipitishwa kwenye korido yenye kunuka harufu ya damu mbichi na kisha kuingizwa kwenye chumba cha kufanana na hoteli ya hadhi, chumba ambacho nilikutana na mzee ambaye nilikuwa namfahamu kama Hudini kutokana na sauti yake. Mzee ambaye tulianza maongezi kwa kunikabidhi picha mbili zenye utata. Moja ikionyeaha watu wanne mmoja nikimtambua kama Rais wa Tanzania Albert Kafumu na walinzi wake wawili wakiwa na mwanaume mmoja wa kizungu wa umri wa makamo kwenye eneo la kufanana na bandari. Picha ya pili ambayo ilinishangaza sana ilimuonyesha mtu huyo miaka mingi iliyopita akiwa kwenye picha ya pamoja na Cheupe akiwa mtoto na baba yake.



    Katika maongezi yetu Hudini alionekana hakuwa anajua zaidi yangu kuhusu fumbo ambalo baba yangu alikuwa anataka niling’amue au labda alikuwa anafanya kusudi kutoniambia… kitu pekee ambacho alinieleza ni kwamba ananikabidhi maagizo kama ambavyo alielekezwa na hana la zaidi ambalo atanieleza. Alinikabidhi tu bahasha yenye nyaraka nyingi ndani yake na kisha kunieleza kuwa atanitafuta baada ya wiki mbili kunikabidhi bahasha nyingine. Nilipomuuliza natakiwa kufanya nini ndani ya wiki mbili hizobili, alinijibu huku anatabasamu kifedhuli… “I don’t know… I am just following my orders!” Na nilipomuuliza hizo “orders” zinatoka kwa nani alinijibu, “its none of your business.!”

    Kwa mtindo ule ule wa walionichukua kutoka mtaa wa Hardstrasse, ndivyo ambavyo walinirudisha… lakini hawakunirudisha pale mtaa wa Hardstrasse bali walinirudisha hotelini nilipofikia karibu na uwanja wa ndege wa Zurich.



    Kutokana na purukushani hizi za kunichukua na kunipeleka kule mtaa wa Wipkingen kutokea usiku wa manane, waliponirudisha hotelini tayari kulikuwa kunapambazuka. Ilikuwa ni asubuhi alafajiri. Kabla ya kuifungua ile bahasha niliyopewa na Hudini kwamba ilinipasa kulala ili kuweka akili yangu sawa. Nilikuwa najihisi kama nina karibia siku tatu sijapata usingizi. Na hakika ilikuwa ni zaidi ya siku tatu. Kuanzia safari yangu ya zaidi ya masaa kumi na sita kutoka Tanzania mpaka hapa Uswisi. Jumlisha usiku nilioenda kwenye mgahawa wa kichina na kufanyiwa mambo niliyopoteza fahamu na baadae kuamka kwenye jengo ambalo silifahamu mtaani Hardstrasse. Na baadae kupelekwa Wipkingen kuonana na Hudini. Kichwa kilikuwa kizito na kilikuwa kinauma haswa nilihitaji kupumzika kwa masaa kadhaa.



    Nakumbuka nililala kwa siku nzima. Kuna muda nilihisi nilikuwa nalala tu sitamani kuamka kwa kuwa sikuwa nataka kukabiliana na uhalisia uliokuwa unanisubiri pindi nikiamka. Lakini hakuna marefu yasiyo na ncha na siwezi kulala milele. Hatimaye jioni yake niliamka na kufungua ile bahasha ambayo nilipewa na Hudini. Nilipoifungua na kusoma zile nyaraka zilizomo ndani nilielewa kwanini roho yangu ilikuwa nzito na kulala siku nzima bila kutamani kuamka. Nilielewa roho rangu ilikuwa inaogopa kukutana na uhalisia wa aina gani. Uamuzi ambao nilichukua baada ya kusoma zile nyaraka ndizo ambazo zimenifanya kuingia kwenye dhahama kubwa kwenye nchi hii ya ugenini niliyopo.



    Lakini hayo yote yalikuwa ni siku mbili zilizopita. Leo hii nilikuwa nakabiliana na uhalisia mkubwa zaidi. Uhalisia wa kama nitathubutu kufumba macho basi kuna uwezekano mkubwa sitayafumbua tena. Uhalisia wa kiza kinene mbele yangu. Uhalisia wa kifo.



    Nikatabasamu tena. Machozi yalitiririka tena kwenye kona za macho. Nikainua tena mkono kutoka tumboni na kuangalia namna ulivyoloa damu. Nikaurudisha tena tumboni kujishika damu isitoke kwa kasi zaidi. Macho yalikuwa yanazidi kulegea na nuru kupotea. Maumivu yote yalikuwa yamepotea. Sio kwamba hayakuwepo lakini mwili wangu ulikuwa unakufa ganzi na nilikuwa siyasikii kabisa. Uhalisia ni kwamba nilikuwa hata sihisi mwili wangu mwenyewe. Kitu pekee ambacho nilikihisi, kitu pekee ambacho kilikuwa ni halisi kwa sasa ni woga. Woga wa uhalisia kwamba nikifumba macho tu sasa hivi hakika sitafumbua tena.



    Nikaanza kufikiria hatua kwa hatua mpaka mahali hapa nilipo muda huu. Sikuwa hotelini, na nina zaidi ya masaa ishirini na nne sijui kitanda cha hoteli yangu. Kwa uzuri zaidi niseme sijakiona kitanda cha hoteli yangu tangu juzi niliporejeshwa hotelini alfajiri na vijana wa Hudini na kisha kulala siku nzima mpaka jioni. Nipo koridoni mwa jengo ambalo visanga na vitimbi vyote vilikoanzia, jengo la HARDSTARASSE 201, 1985. Jengo ambalo siku kadhaa zilizopita nilijikita nimeamka ndani yake. Jengo ambalo nilisikiliza kipande cha video cha ujumbe ambao uliachwa na marehemu baba yangu. Jengo ambalo nilikuta nyaraka kwenye vault ndogo zikionyesha kwamba ninalimiliki. Hapa ndipo nilipo muda huu. Kwenye korido nje ya mlango wa kuingia kwenye kile chumba ambacho siku kadhaa niliamka ndani yake.



    Nilikuwa nimelala hapa koridoni nikihesabu sekunde zilizobakia za uhai wangu. Nilikuwa nimelala nikiwa na jeraha la risasi tumboni linalovuja damu.



    Japokuwa mwili ulikuwa umeishiwa nguvu na hata akili yangu kushindwa kufikiria sawa sawa nikiona maluweluwe tu, lakini nilijitahidi kuwaza. Kuwaza ni nini hasa kilikuwa nyuma ya pazia. Kuwaza nimewezaje kutegeka kirahisi hivi?



    Niliwaza kweli kweli, ni nani hasa alikuwa nyuma ya pazia ya hiki kilichofanyika? Hudini? Lakini akili yangu ilikataa… Hudini alikuwa na uwezo wa kuniua Kyle Wipkingen kama angekuwa na nia hiyo. Lakini kila nilipotaka kumsafisha kichwani mwangu Hudini, akili ilikataa…. Hudini ndiye pekee anayejua uwepo wangu hapa Zurich. Au labda kuna mwingine? Ndio… nilijijibu mwenyewe… yule mzee wa kichina na vijana wake? Inawezekana wao ndio walikuwa nyuma ya pazia? Hapana… akili yangu ilikataa… nao walikuwa na uwezo wa kuniua siku ile ambayo walinipotezesha fahamu kwa kunichoma sindano ya kemikali.! Au kuna mwingine anayefahamu uwepo wangu hapa Zurich bila mimi kujua?



    Ghafla nikasikia mlango wa komeo wa kule nje wa kutoka kwenye uchochoro, nikasikia unafunguliwa kwa staili ile ile niliyoisikia mara ya kwanza kabla ya kupigwa risasi. Macho yangu yaliyokuwa yanasinzia kwa kuchoka kutokana na mwili kuishiwa nguvu, niliyatoa kama vile nimekabwa. Woga ambao niliusikia ulikwa halisi mpaka niliweza kuuhisi kwenye ngozi yangu ya mwili. Kifo kilikuwa halisi mbele yangu kuliko hata nilivyohisi mwili wangu.



    “Huu hauwezi kuwa mwisho wangu.!”



    Nikajifariji japo nilikuwa siwezi hata kuinuka kupiga hatua moja.





    Siku hii ndipo ambapo niligundua kuwa hakuna kitu imara juu ya uso wa dunia kushinda roho ya binadamu. Haijalishi kuna tumaini dogo kiasi gani, lakini roho ya binadamu ina uwezo wa kuhuisha tumaini hilo na kulifanya tumaini kubwa kuliko uhalisia.



    Niliposikia ile sauti ya komeo kufunguliwa kule nje kwenye mlango ambao unatokea uchochoroni, nilijiapiza kuwa safari hii sitasubiri niuwawe hivi hivi. Nitapambana. Kwa kuwa nilikiwa katikati ya korido kama ningelisema nijikongoje ili nijifungie kule ndani kwenye chumba kulikuwa na umbali mkubwa zaidi kutoka hapa ambapo nipo mpaka kufikia ulipo mlango wa kuingia kwenye kile chumba. Lakini nilikuwa karibu zaidi na mlango wa ule ambao unatoka nje. Kwa hiyo kichwani mwangu nikajiapiza kwamba safari hii nitapambana.



    Sijui nilipataje nguvu, ninachokumbuka ni kwamba katika hali hii ya kupigania uhai wangu, katika hali hii ya eidha kufa au kupona nilijikuta napata nguvu ya kujiburuza kuelekea kwenye ule mlango unaotoka nje. Kutokana na kuvuja damu nyingi macho yalikuwa yelegea na nilokuwa naona nusu na nusu sioni, lakini nilijiburuza mpaka mlango ulipo. Kutokana na jengo hili kutokuwa linatumika kwa muda mrefu lilikuwa na takataka nyingi njiani hapa koridoni. Nikiwa najiburuza kuelekea mlangoni nilifanikiwa kuokota kipande cha kamba. Sikumbuki sawia ilikuwa ni kamba ya namna gani lakini ilikuwa kama vile imetengenezwa kwa plastiki na ilikuwa ngumu kiasi chake. Nikaishikilia hii kamba mkononi na kujiburuza mpaka nikafika nyuma ya mlango wa kutokea nje na kujibanza. Mkakati wangu ulikuwa ni kwamba mtu huyu yeyote ambaye alikuwa anajaribu kuja kunidhuru nitamuwahi na kumnyonga kwa hii kamba kabla ajatimiza azma yake dhidi yangu.





    Nikajibanza kimya kabisa nyuma ya mlango. Nilikuwa nusu na ufahamu na nusu nilikuwa sijitambui. Nilikuwa nimepoteza damu nyingi sana.



    Huyu mtu ambaye alikuwa anafungua mlango huko nje ilikuwa dhahiri kwamba hakuwa na funguo kutokana na kuhangaika sana kufungua mlango. Nilikuwa na hakika kabisa alikuwa anajitahidi kufungua kufuli kwa magendo kwa kutumia nyaya au vijiti vya chuma bila funguo. Nikaanza kukiuliza kichwani… huyu ambaye alikuwa anafungua mlango niliamini kabisa ndiye yule ambaye alinipiga risasi… sasa inakiwaje aliufunga mlango akijua kabisa hana fungua na kwamba atahitaji kurudi tena? Au labda kwa namna fulani amegundua kwamba risasi ambayo alinipiga haikuniua kwa hiyo amerejea kuja kumaliza kazi?



    Nikajibanza kusubiri. Jasho lilikuwa linanitoka kweli kweli. Macho yalikuwa yanataka kifumba lakini nikajikaza yasifumbe. Kimoyo moyo nikasema tena ile kauli ya kujipa moyo.



    “Huu hauwezi kuwa mwisho wangu”





    Mlango ukafunguliwa taratibu na mtu ambaye hakuonekana kuwa na haraka. Taratibu nikaona anakanyaga hatua ya kwanza kuingia ndani.



    Kwa nguvu zangu zote ambazo zilibakia mwilini, nilifaytua miguu yangu kumkata mtama baada ya kuona miguu yake yote amekanyaga ndani.



    “Woo wooo!”



    Nilimsikia analalamika kwa taharuki kana kwamba alikuwa hatarajii kushambuliwa.

    Mwili ukiwa umeniishia nguvu hivyo hivyo nikajipa juu yake na kupeleka mkono shingoni mwake ili nimkabe.

    [7/16, 23:49] The Bold: Sikuwa na nguvu za kutosha ili kumkaba nikajikuta naishia kumgusagusa tu shingo.



    “Woo woo! Chill out mate… chill out! I am Jimmy chill mate!”



    Akaongea kwa kusisitiza kana kwamba kunitajia jina lake kulikuwa na maana fulani hivi ya kunituliza munkari yangu.



    “Who are you? What are doing here?” Nikauliza kwa sauti kama ya kilevi hivi kutokana na mwili kuishiwa nguvu kabisa.



    “Chill mate! I am Jimmy… this is Jimmy!”



    Nikamsikia anajitetea tena kwa kunitajia jina lake ambalo kwangu halikuwa na maana yoyote ile.

    Kitu pekee ambacho nilikitambua ni kwamba mtu huyu hakuwa na hatari yoyote kwangu japo nilikiwa simtambui na wala sikujua kwa nini alikuwa hapa.



    Nilimkazia macho kumwangalia usoni kwa usahihi zaidi. Alikuwa ni mtu fulani ambaye hakuwa nadhifu. Mwanaume wa chotara wa kizungu mwenye uasia kwa mbali. Uso wake ulikuwa umechakaa japokuwa hakuwa mzee.



    Kichwani nilijitahidi kuwaza tena na tena ni nini huyu?



    Kabla hajaingia humu ndani nilikuwa na hakika kabisa kuwa mtu huyu mtu alikuwa amekuja hapa ili kunidhuru baada ya kugundua risasi ambayo alikuwa amenipiga mara ya kwanza haikuniua papo papo hapo, lakini sasa kwa muonekano wa huyu mtu tu kwa kumuangalia haraka haraka nilihisi kwa asilimia kubwa mtu huyu alikuwa ni chokoraa wa mtaani, mtu asiye na makazi.



    Nilijikuta najiuliza tena na tena alikuwa amekuja kufanya nini hapa? Masaa kadhaa yaliyopita yametokea mfululizo wa matukio yaliyonifanya nirudi tena kwenye jengo hili na kusababisha nipigwe risasi. Sasa hivi kwa mazingira ya kutatanisha Chokoraa anaingia humu ndani? Hii ni ‘coincidence’? Au kuna mpango fulani wa kunichezea akili?



    “Hey mate! Are you OK?”



    Yule mtu aliongea huku ananiondoa juu yake nilipokuwa nimemlalia kwa lengo la kumshambulia. Mwili ulikuwa umeisha nguvu kabisa. Sikuweza hata kuleta upinzani alipokuwa ananitoa juu yake.



    “You are bleeding badly mate! You need a doctor!”



    Akaendelea kuongea huku akiniegemeza ukutani. Lafudhi yake na maneno waliyokuwa anaongea yakinifanya nihisi kwamba mtu huyu hakuwa mwenyeji wa miaka mingi hapa Zurich au sehemu yoyote ya hapa Uswisi. Lafudhi yake ilikuwa ni ya Uibgereza na hata maneno anayotumia, mfano neno ‘mate’ kwenye kila sentensi ni namna ambayo waingereza wengi ndivyo wanavyoongea.



    Maswali yakazidi zaidi kichwani mwangu!



    Inamaana huyu ni raia wa Uingereza aliyegeuka chokoraa nchini uswisi? Inawezekanaje hii? Na kama hiyo haitoshi kwa mazingira ya ajabu tu ametokea kuingia kwenye jengo ambalo mimi nimo na nimepigwa risasi dakika kadhaa tu zilizopita.



    “Hey mate! We need to get you to a hospital… you need a doctor mate.!”



    Aliongea tena yule mtu huku akinitingisha tingisha kichwani nisilale na kupoteza fahamu. Nilijiegemeza tu pale ukutani aliponilaza nikiwa nusu na fahamu na nusu nikiwa ufahamu haupo kabisa.



    “What happened to you mate??”



    Aliongea akiwa amechanganyikiwa akijishika kichwa huku anashangaa jinsi damu ilivyotapaa pale koridoni.



    “What happened? We need to get you to a hospital mate!”



    Aliongea tena kwa kuchanganyikiwa huku amejishika kichwa anatazama damu zilizotapakaa kila sehemu kwenye korido.



    “No…no…don’t take me to a hospital… please! Don’t take me…to…hospital!”



    Niliongea kwa taabu sana na kwa kujikakakua.



    “Are you crazy why not!! You need a doctor mate!”



    Yule jamaa alisisitiza tena.



    Kwa matukio ambayo yamenitokea kwa masaa 24 yaliyopita sikudhani kama hospitali itakuwa mahala sahihi mimi kupelekwa. Kwanza kabisa sikutaka kuulizwa na maafisa wa serikali ilikuwaje mpaka nikapigwa risasi. Swali hilo lingeweza kujaribu kila kitu na labda hata safari yangu hapa Zurich ikawa haina maana kabisa.



    “Please… don’t… take… to… a…. hospital.!”



    Nikaongea tena kwa taabu sana.



    “You are insane mate! You need a doctor!”



    Aliongea tena akiwa amechachawa huku amejishika kichwa akitembea huku na huko pale koridoni.



    Nikajikuta naanza kujiuliza tena huyu mtu ni nini hasa. Ni chokoraa kweli kama anavyoonekana au labda ni mtego tu? Mwingereza Chokoraa ndani ya Zurich, Uswisi? Na kwa sababu zisizoeleweka amekuja kutokea mahala ambapo nimepigwa risasi ambapo ningekufa na kuoza kwa miezi bila yeyote kujua?



    Nilimwangalia tena na tena kwa umakini zaidi. Macho yalikuwa yamelegea kabisa yanataka kufumba lakini nilijitahidi kuyaakaza niweze kuangalia. Alikuwa amevalia nguo za hovyo hovyo sana ambazo nilianza kuzisikia zikitoa harufu fulani kali kuonyesha kwamba inawezekana zilikuwa hazijafuliwa kwa muda mrefu kidogo.



    “Who are….” Nilishindwa kumalizia sentesi yote, mwili wote uliisha nguvu, macho yakafumba. Kiza kilitanda kila mahala. Kila nilivyojaribu kuyafungua macho haikuwezekana. Kiza kikatanda zaidi. Sikujua kama nilikuwa nalala usingizi au ndio uhai ulikuwa unaondoka. Sikuelewa kilichoendelea. Macho yakafumba kabisa. Ufahamu ukapotea.









    Nilikuwa nasikia baridi kali licha ya kuyahisi mashuka mazito ambayo nilikuwa nimefunikwa. Nilifumbua macho kuhisi mwanga hafifu uliokuwa unapenyeza hapa nilipo kuonyesha kwamba ilikuwa ni asubuhi au mchana kumepambazuka.



    Kichwa kilikuwa kinaniuma na nilikuwa nakisikia kikiwa chepesi sana. Nikajaribu kujiinua lakini maumivu makali tumboni yakanifanya nijilaze tena pale chini. Nilipoyasikia haya maumivu tumboni ndipo ambapo kumbukumbu ya jana ilianza kunirejea kichwani. Kwanza yule ambaye alinipiga risasi na baadae yule chokoraa ambaye niliongea naye kabla sijapoteza fahamu.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Nikaangalia kwa usahihi zaidi hapa nilipo, nilikuwa pale pale koridoni ambapo nilipigwa risasi jana usiku. Kichwani bado nilikuwa na kumbukumbu ya damu ambazo zilikuwa zimetapakaa pale koridoni jana usiku, lakini sasa hivi kila ambavyo nilipepesa macho kutazama sikuona damu hata tone moja. Kwa haraka haraka palionekana kama vile mtu alipapiga deki kwa uzuri kabisa kuondoa damu yote.



    Nikanyoosha mkono tumboni kugusa eneo lile ambalo nilikuwa nimepigwa risasi jana usiku. Nilihisi kama bandeji nimefungwa sehemu hiyo. Ilinibidi nifunue shuka ili nipate kuhakikisha kama kweli ilikuwa ni bandeji ama kitu gani. Nilifunua shuka kuu kuu ambalo nilikuwa nimefunikwa na kukuta kwa hakika kabisa ni kweli ilikuwa ni bandeji. Nilionekana nilikuwa nimesafishwa kidonda vizuri kupatiwa matibabu na hatimaye kufungwa hiyo bandeji.



    Nilitamani kukaa kitako ili nifikiri sawa sawa kuhusu ni nani hasa amenifunga bandeji hii lakini maumivu tumboni yalinilazimisha nijilaze tena chini sakafuni. Kuna shuka lingine kuu kuu lilikuwa limevingirishwa vingirishwa na kisha kuwekewa kichwani nilalie kama mto.



    Niliwaza na kuwazua. Ni nani hasa alikuwa amenipa matibabu ya jeraha langu la risasi? Yule chokoraa? Haikuingia akilini kabisa.



    Nikiwa naendelea kuwaza hivi ghafla nilisikia mlango ule wa kutokea nje uchochoroni unafunguliwa. Safari hii hakufunguliwa kwa tabu. Ulifunguliwa kama vile mtu ambaye alikuwa anafungua alikuwa na funguo au kufuli haikufungwa. Baada ya mlango kufunguliwa hatua ambazo nilisikia zinapigwa kuingia ndani koridoni zilisikika kama vile zilikuwa hatua za watu zaidi ya mmoja.



    Sikusogea wala kutingishika. Nilikaa pale pale nilipo bila hata kujitingisha nikisubiria kuona hao ambao walikuwa wanaingia.

    Ndani ya sekunde kadhaa walikuwa tayari wametokezea hapa koridoni. Hapa ambapo nilikuwa nimejikuta nimeamka nikiwa nimelazwa kwenye mashuka makuu kuu kulikuwa ni mwishoni kabisa mwa korido. Kwa hiyo walipotokezea tu koridoni walikiwa mwisho wa upande mwingine mwa korido. Katikati yetu kukikuwa na umbali usiopungua mita kama tano hivi. Walikuwa ni wanaume wawili, mmoja nilimtambua alikuwa ni yule mtu wa jana usiku ambaye nilimuhisi kuwa ni chokoraa japo nilimuona gizani jana usiku lakini niliweza kumtambua muda huu wa mchana kweupe.



    Alikuwa ni mwanaume wa kizungu wa umri wa makamo, kama miaka arobaini hivi au arobaini na mbili. Alikuwa na nywele nyeusi za singa za asili ya kiasia ya mashariki au kusini ambazo zilikuwa ndefu kiasi zikiwa na muonekano wa wazi kabisa kwamba hazikuwa zinatunzwa vizuri. Mwenzake ambaye alikuwa amekuja naye alionekana mkubwa zaidi kwa umri, labda katikati ya miaka hamsini… kwenye hamsini na nne hadi hamsini na sita hivi. Nywele zake za singa za kizungu zilikuwa zimekatwa kwa urefu wa wastani pamoja na ndevu za wastani kidevuni.



    Yule jamaa ninaye muhisi kuwa ni chokoraa ambaye tulionana tangu jana usiku alikuwa amevalia suruali kuu kuu ya jinzi na fulana nyeusi ya mikono mirefu. Mwenzake huyu aliyekuja naye alikuwa amevaa kwa unadhifu kabisa, amevalia jinzi ya bluu na fulana nyeupe ambayo juu yake alivalia jaketi jeusi la ngozi.



    Walialsimama pale mbele yangu tukiangaliana kwa takribani dakika mbili nzima bila yeyote kati yetu kusema neno.



    “It’s not him!” Yule jamaa nadhifu alimuambia mwenzake yule ambaye nilikuwa nahisi ni chokoraa.



    “You sure mate?” Yule jamaa akajibu kwa kunong’ona.



    “I am hundred percent sure! Its not him…” akamwambia tena.



    Wakageuka kunitazama tena. Walinitazama kwa kuanzia juu kichwani na mwili wote. Walinitazama kwa kunikazia macho kana kwamba walikuwa wananifananisha na mtu fulani hivi au kitu fulani.



    Kuna muda tulijikuta macho yangu na huyu jamaa nadhifu yakagongana. Kuna kitu fulani rohoni mwangu kilikuwa kinanitatiza kuhusu huyu jamaa. Huyu ambaye amevaa nadhifu. Kuna jambo rohoni mwangu lilikuwa linang’amuliwa lakini sikuweza kulipambanua akilini mwangu na kulielewa.



    “So what do I do with him?” Yule chokoraa akamuuliza yule mwenzake nadhifu.



    “Leave him here! Go on with your life.” Yule jamaa nadhifu akajibu bila kumuangalia mwenzake huku akiingiza mkono mfukoni mwake kutoa kitu.



    “What? You are insane mate… he gonn’ die if I leave him here!” Yule chokoraa aliongea huku ametumbua macho.



    “Its non of your business… leave him here!” Yule jamaa nadhifu aliongea huku ametoa wallet kutoka kwenye mfuko wa nyuma wa jinzi na kuhesabu noti kadhaa na kisha kumpa yule chokoraa.



    Nilikuwa nawaangalia tu namna wanavyobisha na kuongea kana kwamba siko hapa. Sikuwa nataka kusema neno lolote lile wala kuuliza chochote. Lakini kwa hiki nilichokisikia tu wanaongea nilijua kwa hakika kabisa kwamba huyu chokoraa jana hakunikuta hapa kwa bahati mbaya. Kulikuwa na kitu cha ziada ambacho kilikuwa kinaendelea. Japo haya maongezi yao yalikuwa yananitisha lakini sikutaka kusema chochote ili nisiwakatishe hiki ambacho walikuwa wananizungumza ili nisikie vya kutosha na nianze kuunga nukta kichwani mwangu.



    Kile kitu kinachofurukuta rohoni mwangu kiliendelea. Kila nilipomwangalia yule jamaa nadhifu kuna jambo lilikuwa linajengeka kichwani lakini sikuweza kung’amua ni kitu gani.



    Yule jamaa nadhifu baada ya kumkabidhi zile noti mwenzake chokoraa aligeuka na kuanza kuondoka. Yule chokoraa aligeuka na kuanza kuniangalia kwa huruma. Alikuwa ananinagalia katika namna ambayo macho yake tu na uso wake niliweza kusoma kile ambacho alikuwa anataka kukisema lakini alikuwa hakisemi. “Natamani nikusaidie lakini siwezi”.



    Akiwa ananiangalia hivi huku yule mwenzake akiwa anakaribia kutokomea kutoka hapa koridoni ghafla tu kichwani nikang’amua kile ambacho kilikuwa kinanikorofisha rohoni kuhusu huyu jamaa nadhifu. Yalikuwa ni yale mavazi yake, na mahususi lile jaketi lake jeusi la ngozi. Lilifanana kabisa na wale vijana wa Hudini, vijana ambao walionekana kama walikuwa walinzi wake ambao siku tatu zilizopota walikuja kunichukua barabarani karibu na jengo hili na kunipeleka maeneo ya Wipkingen kwenye jumba ambalo sikulijua mpaka leo hii, jumba lenye harufu ya damu mbichi. Vijana wale wa Hudini wote walikuwa wamenyoa upara na walikuwa wamevalia majaketi meusi ya ngozi ya kufanana kabisa na jaketi ambalo jamaa huyu alikuwa amevaa. Tofauti yake pekee huyu jamaa alikuwa na umri mkubwa zaidi tofauti na wale vijana wa pia yeye kichwani hakuwa na upara.



    Nilikuwa nimeyasikia maongezi yao ambayo walikuwa wanabishana, huyu jamaa nadhifu na yule chokoraa. Yule jamaa nadhifu alikuwa ameamuru kuwa kwa kuwa huyo anayemuhitaji si mimi basi waniache hapa na kuondoka zao. Na hawakuwa wa wanafanya utani. Walikuwa wameanza kuondoka kweli. Kama wataniacha hapa nikiwa na hali hii nisingeweza kutoka hapa na hakika peke yangu nisingeweza kukabiliana na kifo ambacho ni jana usiku tu kilinikosakosa.



    Japokuwa watu hawa sikuwa nawaelewa hasa ni akina nani na wala sikuwa nawaamini lakini kwa hakika kabisa kama nilitaka kuishi watu hawa walikuwa pengine ndio fursa pekee niliyokuwa nayo.



    Nikakata shauri kichwani kwamba nisilaze damu, nifanye chochote hapa ili kuokoa maisha yangu hata kama ni kitu cha kijinga au kitu cha kuhatarisha maisha yangu.



    “I know Hudini.!” Nikaongea kwa sauti kubwa kwa kujitutumua hasa japo kwa sauti ya uchovu kutokana na maumivu tumboni.



    Wote wawili wakiwa wanatembea kutoka hapa koridoni, yule jamaa nadhifu na yule chokoraa walisimama ghafla na kugeuka.



    Yule nadhifu alipogeuka alikuwa na taharuki kubwa usoni tofauti na yule chokoraa ambaye uso wake haukuonyesha chochote kile. Taharuki yake ilikuwa ni kana kwamba amesikia siri kubwa ambayo haipaswi kusikika kokote.



    “What did you say?” Yule jamaa nadhifu aliniuliza bado akiwa na mshangao.



    Sikujibu chochote. Moyoni nilijipa ‘tano’. Jiwe nililorusha lilikuwa limetua sawia kwa mlengwa. Nilimuona namna ambayo alijawa na mshangao usoni. Namna ambavyo ghafla tu alibadilika kutoka kuwa kwenye mtu mwenye kujiamini kupitiliza mpaka kuwa katika hali ya kuhitaji kujua kile ambacho nilikuwa nakijua.



    Alipogeuka aliganda kwa karibia dakika nzima akichakata kichwani kile ambacho nilikiwa nimekiongea. Kwa namna fulani niliweza kuhisi namna ambavyo sentesi yangu ilikuwa imemchanganya. Inaonekana ni kitu ambacho hakukitegemea kabisa. Kwa namna fulani pia niliweza kuhisi uoga usoni mwake, hakuwa ananiogopa mimi bali alionyesha kuwa alikuwa anaogopa kile ambacho nilikiwa nakifahamu. Na nilidhamiria nimtese haswa. Sio kumtesa kwa mwili wake, bali nimtese kisaikolojia.



    Hakujua kwamba kile ambacho nilikitamka nilitamka kwa bahati tu baada ya kuhisi ile jaketi yake inafanana kabisa na zile jaketi za vijana wa Hudini. Lakini nilitaka nimuache katika hali hii hii, aamini kwamba nafahamu zaidi. Nimuache kwenye hali hii hii na niwatumie kujinasua kwenye haya masaibu ambayo niko nayo.



    “What did you just said?” Yule jamaa nadhifu aliuliza tena kwa taharuki huku akianza kupiga hatua kurejea pale ambapo nimejilaza.



    “Nothing.!” Nikamjibu kwa kifupi na kugeukia pembeni.



    “No no no! What do you know about Hudini?” Akaniuliza tena safari hii akiwa ametembea na kusogea karibu yangu kabisa.



    “Is it him?” Yule Chokoraa naye alikuja kwa hatua za haraka huku anatabasamu.



    Mwenzake hakumjibu chochote. Tulikuwa tumegongesha macho tukiangaliana.



    “I asked you, what do you know about Hudini?” Akarudia tena swali lake.



    “I am not going to tell you anything before you tell me who the hell are you.!!” Nilijitutumua na kujaribu kufoka kwa hasira.



    “No no no! First you tell us, who you are mate!” Yule chokoraa akadakia kwa kujitutumua kama vile mtoto mdogo wa shule afanyavyo.



    “I am not going to tell you shit.! I never asked for you to come here… you all came here by yourselves… so you tell me who the hell are you guys!” Nikafoka safari hii kwa hasira za kweli.



    “Why were you here?” Yule jamaa nadhifu akauliza. Safari hii sauti yake haikuwa na woga bali ilikuwa imejaa mamlaka na kujiamini. Ilikuwa kana kwamba kuna ‘taa’ ya ung’amuzi imewaka kichwani mwake. Aliniuliza swali hili la “kwa nini niko hapa” katika namna ambayo alionyesha kuwa alihisi jambo hilo akilifahamu linaweza kumfanya afahamu hicho ambacho alikuwa anahitaji kufahamu.



    Binafsi yangu, nikaanza kuhisi inawezekana kabisa watu hawa walikuwa na mambo yao mengine tu na walinikuta hapa kwa bahati mbaya. Kwa sababu kilichokuwa kinanishangaza ni kitendo cha wao kutonijua mimi ni nani na nilikuwa hapa kwa ajili gani.



    Lakini kwa upande mwingine wa akili niliwaza… kuna mtu walikuwa wanamtafuta, alikuwa nani? Na kwanini wamtafute kwenye jengo langu? Yes, jengo langu! Kwa mujibu wa ujumbe wa marehemu baba yangu nilioungalia siku tatu zilizopita na zile nyaraka nilizozipata ndani kwenye ile vault ndogo, zilionyesha mimi ndiye mmiliki wa jengo hili kutoka kwa baba yangu.



    Kila nilivyojitahidi kufikirj akili yangu ilikuwa inaniambia kuwa kama watu hawa kama kuna mtu walikuwa wanamtafuta basi nitasema mtu huyo ni mimi, lakini wanaonekana dhahiri walikuwa hawanijui na wala walikuwa hawajui ni kwa nini niko hapa.



    Nikawaza tena labda wana mambo yao, labda wana mtu wao wanamtafuta, labda ni bahati mbaya tu tumekutana. Lakini kila nilipowaza hivi upande mwingine wa akili ulikuwa unakataa. Ni nani amenitibia jeraha langu la risasi? Na kwa nini huyu mtu ameshituka nilipotaja Jina la Hudini?

    Japokuwa alivaa mavazi ya kurandana na vijana wa ulinzi wa Hudini lakini nilihisi bila shaka kabisa huyu hakuwa moja ya timu ya Hudini… kwanza hakuwa na upara kama wenzake na pili vijana wa Hudini wananifahamu kwa kuwa wao ndio walinipeleka kwa Hudini. Sasa kwa nini amevaa mavazi ya kurandana nao? Ni bahati mbaya tu? Haiwezekani kuwa bahati mbaya kwa sababu nilipotaja Hudini ameshituka kama ameona jini.



    Hawa watu ni akina nani? Ni nani wanamtafuta? Kwa nini wako hapa?



    Pia swali ambalo nimeliweka kiporo muda mwingi nalo lilikuwa linanijia kichwani Mara kwa mara, ni nani amenitibia jeraha la risasi?



    “Who are you? What are you doing here?” Yule jamaa nadhifu aliuliza tena safari hii kwa hasira na kujiamini.



    Nikajisemea kimoyo moyo. Liwalo na liwe. Nikatupa karata yangu ya mwisho.



    “I own this place!” Niliongea kwa sauti thabiti ya kujiamini huku nimemkazia macho.



    Mshtuko ambao nilimuona usoni mwake ulikuwa ni kama kwamba mtu aliyetokewa na jini au malaika. Alishtuka mpaka karibia apepesuke adondoke. Niling’amua kwamba jibu langu hili liliwasha taa ndani ya akili yake na ameng’amua jambo.



    “You….!” Aliongea huku anahema bila kumalizia sentesi yake huku ametumbua macho kama mjusi aliyebanwa mlangoni huku mkono mmoja amejishika kifuani kwa taharuki na woga. Aliniangalia kwa mshangao na kwa heshima fulani hivi kwa mara ya kwanza.



    Japokuwa nilifurahi kwamba hatimaye nimeweza kuwateka akili za watu hawa na walikuwa sasa wananiangalia kwa heshima, lakini kwa upande mwingine rohoni nilikiwa na hofu. Nilikuwa nahofia ni kitu gani hasa mtu huyu ameng’amua kutokana na jibu langu?



    Swali langu kiporo nalo likarejea kichwani, hawa watu dakika kadhaa tu zilizopita walikuwa wanaonekana hawanijui… je, ni nani alinitibia lile jeraha la risasi? Kwa nini hakunipeleka hospitali? Je ni huyu chokoraa… ilikuwa haiingii akilini.!







    “Rweyemamu?” Yule jamaa nadhifu alitamka jina langu kwa tabu kwa lafudhi yake ya kingereza huku amejishika mkono kifuani kwa mshangao.



    Kitendo cha kutamka jina langu sio tu kwamba kilinishangaza bali pia kilinichanganya akili. Mtu huyu muda mchache uliopita alikuwa anakaribia kuondoka kwa madai kuwa aliyekuwa wanamtafuta si mimi lakini ghafla tu baada ya kutamka kuwa mimi ni mmiliki wa hili jengo wanaonekana kunifahamu mpaka jina.

    Nilijitahidi nifiche mshangao ambao nilikuwa nao ili niendelee kuyapeleka mazungumzo vile ambavyo nilikuwa nataka.



    “I have been waiting for you for years!” Akatamka sentesi inayofanana kabisa na sentesi ambayo alitamka yule mzee wa kichina kwenye mgahawa. Kwamba kwa miaka kadhaa amekuwa akisubiria kukutana na mimi.



    “Who are you guys?” Nikamuuliza yule jamaa akiwa tayari anainama ili kukaa chini pembeni yangu pale nilipokuwa nimejilaza.



    “I am Luke and this is my friend Jimmy.!” Akajitambulisha na mwenzake wote wakiwa wameketi pembeni yangu. “Jimmy go get us some breakfast!” Akatoa noti nyingine kadhaa mfukoni mwangu na kisha kumpa yule mwenzake ninayemuhisi chokoraa ili aende kununua chakula.



    Maumivu tumboni yalikiwa yamenifanya hata nisahau kama nilikuwa na karibia masaa ishirini na nne sijaweka kitu chochote tumboni.



    Jimmy akapokea hela kutoka kwa Luke na kwenda kuchukua chakula. Tulibaki watu wawili tu hapa koridoni. Mimi na Luke, na nikaona huu ndio wakati hasa wa kunieleza yeye ni nani na nini kilikuwa kinaendelea hapa.



    Nilitumia karibia dakika tano za awali kumshawishi Luke anieleze ukweli kuhusu yeye na kile kinachoendelea ambacho nilikuwa sikijui. Kwa mara kadhaa kila ambavyo nilimshawishi alijaribu kupindisha maongezi kwa kuingiza mjadala kuhusu jeraha langu la risasi na kujifanya kama anajali sana maendeleo yake. Lakini mwishowe nikafanikiwa kumshawishi aongee.



    Aliongea kwa karibia nusu saa nzima, na muda wots huo Jimmy alikuwa bado hajarudi na chakula. Sikujua kama alikuwa ameenda mbali kuchukua chakula au labda walipeana ishara bila mimi kujua kwamba acheleqe kurudi ili mimi na Luke tupate faragha ya kuongea.



    Katika maelezo yake, Luke alinieleza kwamba amewahi kutumikia jeshi kwa kipindi cha miaka nane kabla ya kujiunga kwenye kikundi cha siri kinachofanya kazi ndani ya nchi karibia saba ndani ya ulaya.



    “A fraternity? Secret Society?” Nilimuuliza huku nimemkazia macho.



    Haksema neno lolote lile. Alivua jaketi lake la ngozi na kisha akavua fulana. Kifuani mwake kwenye titi la kushoto kulikuwa na mchoro wa ajabu wa nyoka aliyejinyongorota huku akiwa anateka kitu kama moto. Kitendo cha kuona tu ule mchoro mwili wote ulisisimka.



    “HUDINI.!” aliongea kwa kifupi tu.



    Nilimkodolea macho nikiwa sielewi ni nini hasa alikuwa anajaribu kumaanisha. Jina la yule mzee mwenye lafudhi ya kifaransa linahusiana nini na tatoo yake kifuani.



    “I don’t get your point!” Nilimueleza huku namuangalia kwa sura ya kwamba niko ‘confused’.



    “Its a mark! Each member has one!” Akaongea



    “Member of what?” Nilimuuliza tena



    “HUDINI” akanijibu tena kwa kifupi.



    Kwa mara ya kwanza ndipo akanifafanukia kuwa Hudini si mtu bali ni kikundi cha siri.



    Nilishituka kidogo kwa sababu kwa muda wote huu nilikuwa nadhani kwamba Hudini lilikuwa ni jina la mtu, yule mzee ambaye alinipa picha za Rais Albert Kafumu na yule mzungu na picha za mzungu huyo akiwa na familia ya mke wangu Cheupe.



    Katika maelezo yake alinieleza kwamba kikundi hiki cha Hudini kilikuwa ni kama kampuni ya siri ya kujitegemea ya masuala ya ulinzi, usalama na ujasusi na wanachama wake wote ni wanajeshi wastaafu, majasusi na polisi wachache wa vitengo Maalumu.

    Alinieleza kuwa alitumikia kikundi hiki kwa muda wa miaka ishirini na mbili na kufanikiwa kushika baadhi ya nyadhifa za juu kabisa ndani ya kikundi hicho mpaka miaka miwili iliyopita ambapo alikosana vikali na wenzake na akalazimika kukitoa kwenye kikundi hicho.



    “What happened?”



    Nakumbuka nilimuuliza anieleze kuhusu huo mgogoro ambao ulitokea kati yake na wenzake. Nilimuuliza mara nyingi sana lakini alikataa katakata kunijibu. Kitu pekee ambacho alinieleza tena na tena kila nilipomuuliza ni kwamba, “kuna deni nahitaji kuwalipa?” Ndivyo ambavyo alinijibu kila nilipomuuliza.



    Nilielewa fika kabisa sentensi hii ilikuwa ni fumbo alilokuwa analitumia kumaanisha hicho ambacho aligombana na wenzake.



    Nikaona hakuna maana kwangu kuendelea kumuuliza swali ambalo kamwe hatonijibu na halikuwa na faida yoyote ile kwangu. Nikahamishia maswali yangu kwenye masuala ambayo nilihisi yalikuwa na maslahi ya moja kwa moja kwangu.



    “Why were you looking for me?” Nikamuuliza.



    “Because you are Charles Kajuna’s son.!” Alinijibu huku anatabasamu.



    “So what?” Nikamjibu kwa kukereka kiasi.



    Akaanza kunipa tena maelezo, kwamba alikuwa na uhakika kama akifanikiwa kunipata mimi basi atampata kiongozi wa sasa wa Hudini. Nilipomuuliza kiongozi wa HUDINI anamtaka wa nini, akarejea tena kauli yake ya fumbo, “Kuna deni nataka kuwalipa!”



    Baada ya hapo akaendelea tena kunipa maelezo ambayo kwa kiasi fulani nilikuwa nayajua, kwa usahihi zaidi niseme nilikuwa nimeng’amua mwenyewe baada ya kikao changu cha juzi na yule mzee mwenye lafudhi ya kifaransa ambaye muda wote huu ndiye nilikuwa nikidhani kuwa jina lake alikuwa anaitwa Hudini.



    Luke alinieleza kwamba, katika miaka ya mwishoni ya 1990s mwenyekiti wa jumuiya ya siri ya The Board kutoka nchini Tanzania, yaani baba yangu marehemu Charles Kajuna alitoa kandarasi kwa kikundi hiki cha Hudini kwa ajili ya kazi maalumu. Kazi ambayo ilikuwa ni nadra mno kwa kikundi kama chao kuipata.



    Alinieleza kuwa kikundi chao kilikuwa kwa miaka mingi walikuwa wakipokea kandarasi za kutoa ulinzi kwenye usafirishaji wa biashara za magendo, ulinzi wa wafanyabiashara wakubwa, utekaji wa watu mashuhuri na muda mwingine hata kufanya oparesheni ‘chafu’ za siri za kijeshi kwa niaba ya baadhi ya serikali ambazo zilikuwa hazitaki skendali hizo zije kuchafua serikali zao ikitokea mambo yakafichuka na kuwa hadharani kwenye oparesheni hizo ‘chafu’.



    Alipoongea kuhusu oparesheni ‘chafu’ za siri za kijeshi, nikakumbuka ile picha niliyoonyeshwa ya yule mzungu akiwa na Rais Albert Kafumu wakiongea mafichoni kwenye makontena. Nikajiuliza kama yule mzungu naye ni mwanachama wa Hudini. Hakukuwa na haja ya haraka au papara ya kuuliza maswali. Nikahifadhi swali langu hili moyoni nikamuacha Luke aendelee kuongea.



    Luke akanieleza katika kandarasi hii ambayo walipewa na jumuiya ya The Board, kazi yao ilikuwa kwa macho ya kawaida ilionekana ni rahisi lakini ilikuwa ni kubwa na yenye kuhitaji umahiri na usiri mkubwa kuifanya.

    The Board walikuwa wanahitaji kutunza baadhi ya siri zao kubwa ambazo wao wenyewe The Board walikuwa hawajiamini kuzitunza kutokana na uzito wake. Na si kutunza siri bali pia walihitaji kitu ambacho wenyewe walikuwa wamekiita “REPLACEMENT”. Yaani kama ikitokea jumuiya yao yote imesambaratika basi siri zao hizo zitue kwenye mikono Salama na kuwe na mfumo wa kumuwezesha mtu huyo atakaekabidhiwa siri hizi kufufua tena jumuiya ya kurandana na The Board kama kutakuwa na ulazima wa kufanya hivyo.



    Nikakumbuka ile barua ambayo niliikuta kwenye bahasha niliyopewa na marehemu baba yangu ikiwa na neno moja tu la kifaransa “REMPLACEMENT”. Nikajiuliza mambo kadhaa kichwani. Lakini kwa mara nyingine sikutaka kuwa na papara ya kuuliza swali, nikamuacha Luke aendelee kuongea.



    Luke akanieleza kwamba kutokana na uzito wa suala la The Board, suala hilo lilipaswa kuwekewa mfumo mgumu na wa siri kubwa sana.



    “What was the secret about?” Nilimuuliza kwa kumjaribu.



    Japokuwa nilijua wazi kuwa hata kama angelikuwa anajua asingenieleza kirahisi rahisi namna hii, lakini yeye mwenyewe alinitamkia kuwa hakuwa anafahamu. Alinieleza kwamba baada ya kupokea kandarasi hiyo, viongozi wakuu wa kikundi cha Hudini walitengeneza mfumo wa siri na mgumu kuhusu ‘details’ walizopewa na The Board katika namna ambayo watu wachache tu ndani ya Hudini kila mmoja wao alikuwa anajua details chache tu na hakukuwa na yeyote yule ambaye alifahamu suala hilo kwa ujumla wake.



    Nilihisi hasira fulani hivi moyoni kwamba nkmesafiri maelfu ya maili kutoka nyumbani Tanzania mpaka hapa lakini naambiwa kwamba hata hawa ambao nilitegemea watakuwa na uelewa juu ya kilichonileta hapa nao ati hakuna kati yao anayejua kila kitu.



    “I think i have said enough… its your turn now! What happened to you? How did you get shot?” Akauliza huku anatoa tabasamu hafifu.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Nikakumbuka siku tatu zilizopita niliporejeshwa hotelini kwangu kutoka kule Wipkingen. Nikakumbuka kilichotokea masaa ishirini yaliyopita. Nikajiuliza kama ni sahihi kwangu kumuamini huyu mtu na kumueleza kila ambacho kilitokea. Nikakumbuka msemo wake wa fumbo kuwa “Kuna deni anataka kuwalipa Hudini”. Nikakumbuka alivyoeleza kuwa amekuwa akinitafuta kwa miaka kadhaa kwa kuwa aliamini akinipata mimi atawapata Hudini hasa kiongozi wao wa sasa, ambao alikuwa amekorofishana nao.



    Nikakumbuka namna ambavyo hakunitambua mara ya kwanza na kutaka kuondoka. Nikakumbuka namna ambayo baada ya kumwambia mimi ni mmiliki wa hili jengo aliniita jina langu. Nikajiuliza kama alifahamu jina langu, na pia alifahamu mimi ni mtoto wa Charles kajuna, ameshindwaje kuijua sura yangu? Iweje anitafute miaka yote kama anavyosema na asiwahi kuona hata picha yangu?



    Nikajiuliza tena kwa nini anieleza siri zote hizi. Kuanzia tatoo yake kifuani. Uanachama wake ndani ya Hudini. Shughuli za Hudini na hata ugomvi walio nao na juhudi zake za kuwapata ili “awalipe deni” kama anavyosema.



    Nikajiuliza kama hakuna mtego hapa nimewekewa.



    Nilikuwa nawaza haya huku nimejiinamia. Nikainua uso kumtazama. Alikuwa ananiangalia huku anatabasamu kama vile anaisoma akili yangu.



    “What happened Ray? How did you get shot?” Akauliza tena huku anatabasamu.



    Nikavuta pumzi ndefu na kuishusha. Isingelikuwa jeraha tumboni mwangu, ningeweza kuinuka na kutimua mbio.









    Masaa 36 Yaliyopita…



    Nilikuwa nimetoka usingizini baada ya kulala kwa masaa mengi tangu alfajiri ambapo nilirejeshwa na vijana wa Hudini.



    Baada ya kuoga, kubadili nguo na kuonja kidogo chakula ambacho nilikuwa nimeletewa muda si mrefu na muhudumu wa hoteli nilikaa kitandani na kuanza kuchambua lundo la nyaraka ambazo nilipewa na Hudini siku ya Jana usiku kwenye like jumba lao linalonuka damu. Au niseme mzee ambaye kwa wakati huu nilikuwa nikiamini kwamba jina lake alikuwa ni Hudini.



    Lilikuwa ni lundo la nyaraka pamoja na ile picha ya jamaa wa kizungu akiwa na Rais Albert Kafumu na picha nyingine akiwa na cheupe pamoja na baba yake.



    Nikaziweka picha pembeni na kisha kuanza kupitia hizi nyaraka moja baada ya nyingine. Kwa namna fulani nyaraka hizi zilikuwa zinafanana na zile ambazo nilizikuta kwenye vault ndogo kule kwenye jengo ambalo nilisikiliza ujumbe wa marehemu baba yangu kwenye video.

    Zilikuwa nyaraka ambazo ziliorodhesha umiliki wa mali ambazo nilikiwa sizijui, majengo, akaunti za benki. Pia kulikiwa na lundo la anuani za sehemu mbali mbali ambazo sikuelewa mara moja ni wa wapi na kulikuwa na maana gani.



    Nilipitia nyaraka zote moja baada ya nyingine, lakini mpaka nilipofika karatasi ya mwisho bado nilikuwa naona maluelue tu. Ni kitu gani hasa ambacho nilikuwa natakiwa kukifanyia kazi kwenye nyaraka hizi? Niliona kila kitu orodha ya mali na majengo ambayo siyajui yalipo na wala sijawahi kuyaona. Niliona pia makumi ya namba za akaunti za benki! Napaswa kuchnguza moja baada ya nyingine? Niliona pia mamia ya anuani mbali mbali! Je napaswa pia kuchunguza kila anuani ambayo imeorodheshqa kwenye nyaraka hizi? Si itanibidi kukaa Zurich mwaka mzima?



    “Fuuucckk.!!” Niling’aka peke yangu… huu ni zaidi ya uwendawazimu.



    Nikainuka kutoka kitandani na kuanza kutembea kuelekea dirishani. Pembeni ya dirisha kulikuwa na kijimlango fulani hizi chembamba cha kioo ambacho nilikifungia na kutokezea kwenye ‘balcony’ ya chumba changu cha hoteli.



    Nilisimama kwenye balcony na kuutazama mji wa Zurich. Namna mataa ambavyo yalikuwa yanang’ara usiku kama huu. Kulikuwa na manyunyu fulani ya mvua inayoanza. Kama ingelikuwa siku nyingine, nyakati nyingine ambayo haikuwa na maswali na mafumbo kichwani mwangu kama ilivyo sasa. Kama ingelikuwa siku nyingine Cheupe akiwa pembeni ya ubavu wangu, muonekano huu, kusimama hapa kwenye balcony na kutazama mataa ya Zurich usiku huu ingekuwa ni wasaa wa furaha tele. Lakini kwa muda huu kitu pekee ambacho kilikuwa kinauwezo wa kunipatia furaha na amani ndani ya moyo ni kufumba macho ya kuvuta kumbukumbu. Kumbukumbu ya enzi za utoto, nyumbani kwa shangazi yangu Mwembechai.



    Nikafumba macho kukumbuka namna ambavyo siku ambazo zilikuwa na mvua kama hivi namna asubuhi yake kunavyokuwa kukimya. Namna ambacho jua linachomoza taratibu kujipenyeza dirishani na kumulika usoni kama vile linanijaza uhai wa siku hiyo. Naomna ambavyo asubuhi ya siku ya mvua pazia dirishani inakuwa tulivu kama vile imeninginizwa kwenye nyumba ambayo haina wakazi kwa miaka. Namna ambavyo masikio yanafurahi kusikia sauti hafifu za ndege wa asubuhi wakiimba kutokea mbali. Namna ambavyo bati linadondosha matone magodo ya maji taratibu kutokana manyunyu hafifu ya mvua inayokaribia kukoma.

    Namna ambavyo nikitoka nje siku ya asubuhi ya mvua mtaa wote unakuwa kimya kabisa, mtaa wenye fujo lakini ukionekana kama hauna wakazi. Lakini japokuwa hakuna vingi vya kuviona, kuna vitu lukuki vya kuvihisi.



    “There is much to be felt, and little to be seen.!” Nikatabasamu nikikumbuka msemo wangu huu wa utoto. “There is much to be felt, little to he seen.!” Nikaurudia tena na tena kichwani huku natabasamu.



    Kadiri ambavyo nilikuwa naurudia kichwani ndivyo ambavyo kuna ‘taa’ ilikuwa inawaka kichwani mwangi. “There is much to be felt, little to be seen”. Kuna kitu nilihisi akili yangu imekihisi lakini sikujua ni kitu gani. Nikaurudia tena na tena ule msemo kichwani huku narudi ndani ya chumba cha hoteli. “There is much to be felt, and little to be seen.!”



    Jicho langu lilitua juu ya lundo za nyaraka pale kitandani. ‘Taa’ ikawaka zaidi. Yes, ni hili lundo la nyaraka… nilikuwa nahangaika muda wote kutafuta kitu ndani yake chenye jibu la moja kwa moja kumbe labda ni ‘detail’ ndogo tu ndiyo nilikuwa natakiwa kuifahamu. Detail ambayo yawezekana akili yangu ilishaihisi. Jawabu halikiwa kwenye huu uwingi wa anuani na orodha za akaunti za benki. Bali suala fulani dogo tu. “There is much to be felt, and little to be seen.!” Nikaurudia tena msemo kichwani na kuanza kuzipekea tena kwa pupa.



    Nilihisi kabisa kuna kitu hapa ambacho nilikidharau mwanzoni lakini ndicho ambacho kinaweza kuwa na majawabu ya kila kitu.

    Nikapekua karibia dakika tatu nzima. Hatimaye nikakutana nacho. Au niseme kwa mujibu wangu nilihisi ndicho hicho.



    Kulikuwa na karatasi moja tu ambayo ilikiwa maandishi ambayo uamefutwa kwa wino mweusi na katikati ilikuwa na kapicha kadogo cha ‘black and white’ ambacho kimechapwa kwenye karatasi. Yaani karatasi juu ilikuwa na ‘paragraph’ kadhaa ambazo zimefutwa kwa wino mweusi katika mtindo unaofanana kabisa na karatasi za mambo ya ujasusi na intelijensia huwa zinazibwa maandishi kwa wino mweusi ili kilichiandikwa kisisomwe.

    Katikati kulikuwa na hicho kipicha cha ‘black and white” kisha chini yake kulikuwa na maelezo ambayo nayo yalifutwa kwa wino mweusi.



    Nikaitazama hii picha kwa makini. Ni picha ya eneo. Sehemu ambayo naifahamu kabisa hapa Zurich. Ni ule mgahawa wa kichina ambao nilienda siku ya kwanza na kuchomwa kemikali nikapoteza fahamu. Nikaiangalia picha kwa makini zaidi. Nilikiwa sijakosea ni penyewe.



    Maelezo ya hii picha yalikuwa yamezibwa kwa wino mweusi kama ilivyo kwa paragraph za juu yake. Lakini kwenye maelezo hayo yote yaliyofichwa kulikuwa na neno moja tu limeachwa na nina imani liliachwa kwa makusudi kabisa. Sikuelewa kwa nini liliachwa, na wala sikuelewa lilikuwa lina maanisha nini. Lakini kwenye karatasi hii kila kitu kilikuwa kimefutwa kwa ustadi kwa wino mweusi na kuachwa hii picha na neno moja tu;



    “MELCHIZEDEK ”



    Mvua nje ilikuwa imeshika kasi. Na safari hii nikaanza kuiskia radi ikipiga. Japokuwa mvua ilikuwa ni kubwa na radi lilipiga kwa nguvu lakini kitu nilikuwa nahisi ukimya wa ajabu ndani ya chumba cha hoteli. Kuna hisia mbaya nilianza kuisikia mpaka vinyweleo vilisisimaka. Ule ukimya. Sijui kama ulikuwa ukimya ndani ya chumba cha Hotel au ukimya kwenye nafsi yangu. Lakini nilihisi ukimya kiasi kwamba hata tone la maji linedondoka ningelisikia.

    Kuna kitu hakikuwa sawa humu ndani ya hoteli.



    Nikatazama ile karatasi na maandishi yake yaliyofutwa futwa kwa wino mweusi. Nikatazama ile picha ya mgahawa wa kichina katikati. Nikasoma tena yale maandishi yaliyoachwa.



    ” MELCHIZEDEK ”



    Nilihisi nimepata wazo nianzie wapi kufumbua fumbo lililonileta hapa Zurich. Lakini bado nilipata hisia, kuna kitu hakikuwa sawa ndani ya hiki chumba cha hoteli. Ukimya ndani ya nafsi yangu ambao ulihamia mpaka kwenye chumba nilichomo ulikuwa ni ukimya wa kutisha.









    Mara nyingi sana katika maisha kadiri ambavyo utakuwa unahangaika kutoka kwenye jambo ndivyo ambavyo unakuwa unapalilia kina cha kuzama. Ni kama vile kuzama kwenye bwawa lililojaa tope tupu, kadiri ambavyo utahangaika kujiokoa ndivyo ambavyo unazama zaidi na zaidi.



    Ndivyo namna ambavyo maisha yanakupa kitendawili mara nyingi, kitendawili ambacho jawabu lake ni fumbo na kadiri ambavyo utaling’amua hilo fumbo ndivyo unaingia kwenye sintofahamu ya fumbo kubwa zaidi.



    Unapozama kwenye bawa lenye tope tupu, busara ni ipi? Utulie tu na kushuhudia nafsi yako ikiondokewa na uhai au uhangaike na kuzama zaidi ndani ya tope?



    Ni ajabu kwa kiasi gani maisha yanaweza kugeuka na kuwa uwanja wa mahangaiko… kadiri tunavyohangaika kuboresha maisha yetu ndivyo kadiri ambavyo tunazidisha msongo vichwani.

    Ni ajabu namna gani ambavyo kadiri tunavyojitahidi kujifunza na kufahamu ndivyo ambavyo maswali mengi zaidi yanaibuka vichwani.

    Ni ajabu ni namna gani ambavyo tunapenda ndivyo ambavyo tunazidi kuumiza mioyo yetu.



    Ni ajabu ni namna gani tumezaliwa na kupewa aina ya maisha ambayo hatukuiomba. Maisha ambayo yanahitaji mapambano kuyajaza fahari. Mapambano ambayo muda mwingine yanaweza kuchukua miaka yetu yote ambayo tutaishi hapa duniani.



    Ni ajabu kwa nini tumetengewa maisha ambayo tunayo.!





    Japo tayari zilikuwa zimepita karibia dakika tano tangu nifike nje ya mgahawa huu wa kichina lakini bado nilikiwa nashindwa kufanya uamuzi wa nini hasa cha kufanya.



    Mlango wa mgahawa ulikuwa umefungwa na kibao kilichosomeka “CLOSED” kilikuwa kinaning’inia mlangoni. Japokuwa mgahawa huu mbele ulikuwa na vioo tupu lakini sikuweza kuona ndani kutokana na giza na taa zake kuzimwa. Kuna hisia fulani nilikuwa naipata kwamba kulikuwa na uwezekano mgahawa huu ulikuwa haujafunguliwa kwa siku kadhaa, labda pengine tangu siku ile nilipofika hapa. Haikuwa sawa sawa kwa mgahawa hapa Zurich kufungwa muda huu kwa sababu hata saa tatu usiku ilikuwa haijafika bado.



    Mvua bado ilikiwa inanyesha na nilikiwa naloa nikiwa nimesimama hapa nje ya mgahawa najiuliza ni nini hasa natakiwa kufanya ingawa hata nilikuwa sijui ni kwa nini hasa nilikuwa hapa. Mfukoni mwangu nilikiwa na kijipande cha karatasi nilichokitoa kwenye lile lundo la makabrasha nililoacha hotelini. Nilichukua kipande hiki tu cha karatasi ambacho kilikuwa na maandishi yaliyofutwa futwa yote yakiacha neno moja tu “MELCHIZEDEK”, pamoja na Picha ya mgahawa huu.



    Kwa hiyo sababu pekee ambayo ilikuwa imenileta hapa ilikuwa ni kwa sababu picha yake mgahawa huu ilikuwa kwenye makabrasha ambayo nilikabidhiwa na Hudini. Sikujua ni nini hasa nilikuwa nakitafuta lakini niliamini tu kwamba ingeweza kunifumbua macho juu ya lengo langu la kuwa hapa Zurich.



    Katika muda kama huu ndivyo ambavyo nilijikuta kwa kiwango fulani nilikuwa najuta kwa nini nilikuja hapa Zurich? Nafsi yangu mara kadhaa nilijikuta kama kuna sauti inaniuliza, kwa nini uko hapa?



    Yote kwa ajili ya kukonga kiu yangu ya kutaka kujua. Yote kwa sababu ya kukonga kiu yangu ya fumbo ambalo marehemu baba yangu alinifumba siku ambayo alijitoa uhai wake mbele yangu.

    ” Au labda kuna lingine la zaidi akilini mwangu ambalo naogopa kulikiri hata kwa nafsi yangu mimi mwenyewe?” Nilijikuta najiuliza moyoni mwangu. Kwamba labda kuna jambo la zaidi kuhusu The Board ambalo nafsi yangu ilikuwa imeshawishika lakini nilikuwa nashindwa kukiri ndani ya nafsi yangu.



    Nikaliondoa hilo wazo haraka kichwani mwangu. Nikarejesha akili yangu kwenye lililo mbele yangu, mgahawa huu wa kichina.



    Mvua bado ilikuwa inanyesha kwa fujo, ikimiminika mwilini mwangu kama vile wingu lilikuwa juu ya kichwa changu.



    Kama ilivyo kwa mgahawa mingine yote niliamini kabisa kwamba pia hata mgahawa huu wa kichina lazima nao utakuwa na mlango wa nyuma. Mlango ambao unaenda moja kwa moja jikoni kama ilivyo ada kwenye mgahawa mingine yote.



    Sikuwa na hakika sana mlango huu nilikiwa nauhitaji kwa sababu gani lakini hulka yangu ya kutorudi nyuma ilikuwa inanisukuma kufanya hivyo. Baada ya kufika hapa tu mgahawani japokuwa nimeukuta umefungwa lakini kwa namna nilivyo si jambo ambalo linawezekana kwangu kugeuza na kurudi hotelini kwangu bila kufanya chochote kile.



    Mgahawa huu ulikuwa kwenye Jengo lenye kama ghorofa tano juu ambalo sikujua kama juu lilikuwa linatumika kama makazi ya watu au maofisi. Pembezoni kwa jengo kulikuwa na uchochoro unaoingia na kufanya kama unazunguka nyuma ya jengo. Niliamini kabisa kama kulikuwa na mlango wa nyuma wa kuingia jikoni basi mlango huo utakuwa kwenye uchochoro huu.



    Sikutaka kupoteza muda, nikaanza kutembea kuufuata huu uchochoro.



    Mvua bado ili kuwa inaendelea kunyesha na nilikuwa naendelea kuloa.



    Sauti ya ngurumo ilivyokuwa inapiga, radi ikimetata meta kila baada ya dakika kadhaa, matone yenyewe ya mvua mfululizo, kila kitu kilikuwa kinafanya nafsi yangu kujipa tathimini. Kila tone la mvua ambalo nilikuwa nalisikia likitiririka kutoka kichwani, shavuni na kisha mwilini, yalinikumbusha machozi yote ambayo nimewahi kuyasababisha kwa watu kutokana na maamuzi ambayo nimewagi kuyanfanya na nilijikuta najiuliza kwa hiki ninachokifanya sasa hapa Zurich huko mbeleni nitasababisha machozi kwa watu wangapi?



    Na kila ambapo sauti ya ngurumo ikilia ilinifanya nijisikie hasira. Hasira juu ya nafsi yangu mwenyewe, hasira juu ya maamuzi ninayoyafanya kila siku ambayo yanaweza kuleta vidonda visivyo pona nafsini. Lakini kila baada ya dakika kadhaa radi ilipiga. Japokuwa mwanga wake uliangaza kwa kasi kuweza macho yangu kuufaidi nuru yake, lakini kila muda mwanga wa radi ulipooiga nilijikuta moyoni najipa moyo, najifariji kwamba labda iko nuru mbele, liko tumaini. Kwamba maumivu yote haya yanastahili ilo kufikia nuru hiyo.



    Nikaendelea kuufuata ule uchochoro. Kulikuwa na malundo kadhaa ya mifuko mikubwa ya plastiki, meusi ambayo ilikuwa imejaa taka za vyakula. Moyoni nikajipongeza kuwa nilikuwa sahihi, uchochoro huu ulikuwa unaelekea moja kwa moja kwenye mlango wa nyuma wa mgahawa kuingia jikoni.



    Nikatembea hatua kadhaa kupita ile mifuko ya plastiki ya kuwekea taka. Nilipoipita na kutembea kama hatua tano tu nikakutana na mlango. Mlango wa chuma kama geti dogo tu la kawaida la rangi nyeusi. Nilipoufikia tu mlango bila kujiuliza mara mbili au kufikiri sana nilinyoosha mkono na kuujaribu kufungua. Mlango ulifunguka.



    Nilishangaa. Ilimaanisha kwamba mlango ulikuwa umeegeshwa tu bila kufungwa na funguo. Kwa hiyo ilikuwa na maana kwamba kulikuwa na watu huku ndani jikoni japokuwa mgahawa ulikuwa umefungwa kule mbele.



    Nilipiga hatua na kuanza kuingia ndani kwa tahadhari kubwa sana. Nilihakikisha kuwa kila hatua ambayo nilikuwa nakanyaga chini haikuwa inasikika. Nikaingia ndani na kuufunga mlango kama ambavyo nilikuwa nimeukuta. Ndani taa zilikuwa hazijawashwa hivyo kulikuwa na kiza kikubwa. Nilitamani ninyoonye mkono ukutani kupapasa kutafuta swichi ili niwashe taa, lakini sikutaka kufanya chochote kile tofauti na namna ambavyo nilipakuta hapa ndani kwa kuwa nilihofu uwepo wa watu wengine humu.



    Nilisimama ka karibia dakika mbili kuyapa macho yangu muda wa kuzoea kiasi hali hii ya giza ili niweze kung’amua vitu japo kwa uchache.



    Nikaanza kuona japo kwa mbali sana na kwa uhafifu. Nilikuwa kwenye korido ambayo kama hauta saba kutoka nilipo kulikuwa na mlango unaoingia kulia ambako niliamini kwamba huko ndiko kwenye jiko. Hatua kama tano hivi kutoka mlango huo kulikuwa na mlango mwingine ambao nao ulikuwa mkono wa kulia ambao nao nilihisi kwamba ulikuwa unaelekea mgahawani kule mbele ambako hukaa wateja.





    Mkono wa kushoto kulikuwa na mlango mmoja tu ambao sikujua hasa ulikuwa ni mlango wa nini.



    Nikaanza tena kutembea kwa kunyata nikihakikisha hakuna hata hatua yangu moja ambayo ilikuwa inasikika nikikanyaga hapa sakafuni.



    Nikatembea haraka haraka lakini kwa tahadhari kubwa sana na kisha nikakunja kulia kwenye mlango wa kwanza ambao niliamini kuwa ulikuwa ni mlango wa jikoni. Kutokana na kuukuta ule mlango wa nje uko wazi nilikuwa na imani kubwa sana kuwa japokuwa humu kulikuwa na giza lakini sikuwa peke yangu. Kuna sababu kwa nini mlango ule umeachwa wazi.



    Kutokana na kitete changu cha kutembea haraka haraka, nikajikuta nimekanyaga kitu sakafuni… sijui ilikuwa ni sufuria, sijui ni sahani lakini ninachokumbuka ni kwamba kilitoa mlio mkubwa. Moyo ulipasuka na kutulia kimya kabisa kusikilizia kama nitasikia mtu yeyote anakuja.



    Sikusikia mtu akiwa anakuja, wala sikusikia purukushani yoyote ile, nilishituka tu taa ikiwa imewashwa na kijana wa kichina aliyevalia suti nyeusi na bastola mkononi akiwa amesimama mbele yangu.



    “…#####%%&&&&&&&#…”



    Sikuelewa alichokuwa anakiongea. Alikuwa anaongea kichina kwa jazba huku ameinua bastola na kuninyooshea.

    Nilibakia nimetumbua macho na kuinua mikono huku natetemeka.



    “Don’t shoot. Don’t shoot.!” Niliongea huku nimeinua mikono juu natetemeka.



    “…#&#$&$&#&$…!”



    Aliongea tena kwa jazba bado bastola ikiwa imeelekea upande wangu.



    “Melchizedek.!! I’m looking for Melchizedek.!” Nilijikuta naropoka bila hata kuelewa kama nilikuwa sahihi au ni kwa namna gani kutaja jina hilo la Melchizedek kungenisaidia mchina huyu aliyepandwa na mori asinitandike risasi.



    Lakini nilipotaja tu jina la Melchizedek niligundua kwamba alipatwa na mshituko ghafla usoni.



    “..&$%*##&$##..!” Aliongea kitu fulani hivi kwa kichina lakini alikiongea kwa taratibu huku amenikazia mamcho. Nilihisi alisema “Umesemaje?”



    “Melchizedek.! I’m looking for Melchizedek.!” Nikarudia tena kujibu.



    Hakunisemesha kitu chochote kile. Alinifuata haraka pale nilipo na kunikunja shati kifuani na kuanza kunivuta kutoka mule jikoni.



    Alinivuta huku anatembea haraka mpaka tukafika koridoni. Kote huku nako taa zilikuwa zimewashwa. Aliendelea kunivuta tukauvuka ule mlango unaopinda kulia kwenda mgahawani kwenyewe, alinivuta mpaka kwenye mlango ambao ulikuwa upande wa kushoto. Hakukuwa na chumba bali kulikuwa na ngazi kuelekea ghorofa ya juu.



    Tulipanda ngazi haraka haraka huku akiendelea kunivuta shati kwa nguvu mpaka tukatokezea juu ghorofani ambako mbele yetu kulikuwa na mlango. Akagonga mlango kwa haraka kama kulikuwa na dharura fulani hivi. Mlango ukafunguliwa na akanitutusa na kunitupia ndani.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Kulikuwa na lijichumba likubwa mno. Karibia nusu ya ‘floor’ yote ilikuwa ni lichumba hili au ‘hall’ naweza kusema.



    Kulikuwa na makorokoro mengi sana lakini mengi yakiwa ni maboksi yaliyotengenezwa kwa mbao ambayo sikujua mara moja yalikuwa na nini hasa ndani yake.



    Upande mmoja kulikuwa na meza na kiti kama ofisi na juu ya kiti alikuwa ameketi yule mzee wa kichina. Ni mzeebyule yule ambaye alinichoma sindano ya kemikali siku ya kwanza nilipokuja hapa na nikazimia na kuja kuzinduka nikiwa kwenye jengo kule mtaa wa Hardstrasse. Pamoja na yeye kulikuwa na vijana wengine wenye asili ya kichina kama kumi hivi.





    “….##&&$&##%#&##&…Melchizedeck…!”



    Yule jamaa ambaye alinikwida na kunileta hapa msobesobe alizungumza kichina na nilifanikiwa kung’amua neno “Melchizedek” kwenye sentensi zake.



    Wote mle ndani akiwemo yule mzee wa kichina niliwaona wameshituka ghafla baada ya yule mwenzao kutamka jina la “Melchizedek”.



    Yule mzee wa kichina aligeuka na kunikazia macho kwa karibia dakika tatu bila kusema neno lolote lile. Alikuwa kama anatathimini kitu fulani hivi. Nadhani uwepo wangu hapo na kile ambacho mwenzake alikuwa amemueleza.





    “Is it true?” Aliniuliza bado akiwa amenikazia macho.



    “What? I didn’t understand what he said!” Nikamjibu huku nikijitahidi nionyeshe taswira ya kujiamini.



    “Is it true that Melchizedek sent you here?” Hakupepesa macho hata kwa sekunde. Aliniuliza huku ananiangalia moja kwa moja akiwa amekaza macho.



    Sikuwa na muda wa kufikiri au kutafakari nitoe jibu gani. Kwa jinsi ambavyo alikuwa amenikazia macho kama ningethubutu kutafakari japo kwa sekunde tu basi angehisi nilikuwa nadanganya. Na kwa kuwa hakutaka nidanganye basi nikachukua uamuzi wa kumdanganya. Bila kufikiria sana nikajikuta tu nimeropoka,



    “Yes! Melchizedek sent me here..!!”



    Niliona mshituko wake usoni. Mara moja alisimama kutoka pale kwenye kiti ambako alikuwa ameketi. Sikujua kama ilikuwa ni hasira au alikuwa kwenye mshangao. Nakumbuka tu aliinuka haraka na kwa taharuki na kuanza kutembea kwa haraka kunifuata pale nilipo.



    Nilianza kutamani labda nisingesema uongo. Lakini kwa kuwa tayari nimeshaanza na uongo niliousema basi napaswa kusimamia uongo huo. Lakini mtihani niliokuwa nao ni kwamba hata huyo Melchizedek sikumjua ni nani au anafanya nini au ilikuwa na maana gani.



    Japokuwa mzee huyu anajifanya kufanya biashara ya mgahawa uliopo hapo chini lakini kwa hakika kabisa biashara yake halisi ilikuwa ni suala fulani la hatari au uhalifu kutokana na hawa vijana alionao ambao kwa mtindo ambao walikuwa wamevaa makoti yao ya suti nilikuwa na hakika kabisa kila mmoja wao alikuwa na silaha ya moto kiunoni.



    Mzee alitembea mpaka mbele yangu kabisa tukawa tunaangaliana uso kwa uso.



    “Where is the package?” Aliniuliza huku amenikazia macho na anapumua kwa hasira.



    Nilitamani nimuulize “mzigo gani?” Lakini nikajua kuwa ndio nitaharibu kabisa. Nahitaji kutoka jibu la maana kabla hawajajua nadanganya na hata kile nilichotumaini kukipata hapa ili kinisaidie kwenye hizi harakati zangu nikakikosa.!!





    "Where is the package??" Yule mzee aliniuliza tena kwa kunikazia macho huku ananisogelea karibu baada ya kukaa kimya aliponiuliza mara ya kwanza.



    Nilijua kabisa sipaswi kukakaa kimya, natakiwa nitoe jibu haraka kabla hawaingiwa na wasiwasi wowote na kunitilia mashaka.

    Lakini pia sikutaka kutoa jibu la kukurupuka na kuharibu kabisa. Uhalisia ni kwamba sikuwa nimetumwa na 'Melchizedek' na wala sikufahamu Melchizedek ni nani au kitu gani. Jibu moja tu lisilo sahihi lingesababisha kuharibika kwa kila kitu.



    Nilitamani kumvimbia na kumwambia kuwa "siwezi kumpa mzigo mpaka ajibu maswali yangu" lakini kuna upande fulani wa roho yangu ulikuwa unakataa kutoa jibu la namna hii. Kuna asilimia fulani ndani yangu ilikuwa inaamini kwamba swali hili lilikuwa ni swali la fumbo, swali la utambulisho. Yaani kwamba, kuna namna fulani ambayo wamejiwekea kwamba kama ni kweli wewe ni mtu kutoka kwa 'Melchizedek' basi utajibu swali hili kwa jibu mahususi ambalo wenyewe wamekubaliana liwe hivyo. Kwa maana ya kwamba swali lake hili "where is the package?" Hakuwa hasa anahitaji nimpe mzigo fulani kutoka kwa 'Melchizedek' bali alikuwa anataka nifumbue fumbo!

    Lakini hii yote ilikuwa ni moja tu ya nadharia ambayo nilikuwa naiwaza kichwani mwangu, sikujua hasa kwa uhakika ni jibu gani nitoe, ni nini hasa maana ya swali lake? Ni kweli anataka mzigo kutoka kwa 'Melchizedek' au lilikuwa ni swali la fumbo ambalo nilipaswa kutoa jibu mahususi?



    Yote haya nilikuwa nayafikiria kwa kasi kubwa kichwani mwangu, kama ndani ya sekunde tano tu ndizo ambazo nilitumia kuwaza hii sintofahami kichwani. Yule mzee bado alikuwa amenikazia macho bila kupepesa hata mara moja japo hata kwa sekunde tu.



    "Come on man! Really??" Nikaongea huku navuta mdomo pembeni kuashiria kana kwamba ameuliza swali la kijinga, nikijitahidi kujenga picha kwamba alikuwa anafanya 'utoto' kwa kuniuliza swali la mtego kama hilo kwa kuwa mimi ni 'mwenzao' na twende kwenye mazungumzo moja kwa moja badala ya haya maswali. Lakini pia nilitamka katika namna kwamba kama alikuwa anamaanisha nimpe mzigo kutoka kwa Melchizedek pia alikuwa anafanya 'utoto' kwa kuutaka kirahisi rahisi hivyo! Kwa hiyo niliongea sentesi moja ambayo haikuwa na maana dhahiri moja kwa moja lakini niliamini kwamba tafsiri yake ingetokana na huyu mzee alikuwa na maana gani hasa kwa kuniuliza swali 'where is the package?"



    Mzee wa kichina alinikazia macho zaidi. Hakusema chochote kile, hakupepesa macho wala kuonyesha hisia yoyote ile kana kwamba hakusikia chochote kile ambacho nilikuwa nimeongea.

    Sikutegemea aseme chochote wala kujibu chochote lakini nilitamka nilichokisema ili nijipe walau muda mwingine kiduchu wa kutafakari ni nini haswa ambacho natakiwa kujibu.



    "I'm going to ask you one last time… where is the package?" Aliniuliza huku akiwa serious zaidi safari hii na akiwa amekaza macho kifedhuli kuashiria kwamba uvumilivu wake ulikuwa unakaribia kikomo.



    Kwa namna ambavyo alinitazama nilipoongea sentesi yangu ya kuzugia "come on man, really??" na namna ambavyo safari hii aliuliza tena "where is the package?" Niliamini kwa asilimia kubwa zaidi kwamba hili lilikuwa ni swali la fumbo na nilipaswa kutoa jibu mahususi ili kuthibitisha kwamba ni kweli nimetumwa hapa na 'Melchizedek'.



    Nilitamani kama muda urudi nyuma dakika chache niwe hotelini kwangu na nipange mkakati maridhwa zaidi. Nilihisi nimejiingiza kwenye mtego wa simba bila kujiandaa namna gani ambavyo nitajinasua na kutoka.



    Kwa muda wa kama sekunde kumi tu akili yangu ilifanya kazi kwa haraka na kasi kubwa ili walau nipate cha kutamka mdomoni.

    Ndani ya sekunde hizo hizo kumi sikujua ni nini kilinipata lakini nikajikuta akili yangu inaanza kufikiri juu ya ile picha ya mkewangu Cheupe utotoni akiwa na baba yake na yule bwana mzungu ambaye sijamfahamu mpaka sasa ni nani na ana uhusika gani katika hiki kitendawili kinachonikabilo.

    Lakini akili yangu ilipowaza tu picha ya Cheupe utotoni nikakumbuka namna ambavyo tangu utoto wake baba yake ekuwa akipenda kumita 'malkia'… neno malkia lilipoibuka kichwani mwangu sikujua ni kwanini lakini moja kwa moja nikajikuta nimehisisha malaika na jina hili 'Melchizedek' na nilipounganisha tu vitu hivi viwili 'Melchizedek' na malaika nikajikuta akili yangu inakubali kwamba niko sahihi japokuwa upande mwingine wa akili yangu ilikuwa inaniambia kuwa naota ndoto za mchana.



    Lakini kuna picha nyingine ilikuwa inanijia kichwani, picha ya 'crown', kofia ya kifalme ya kale ambapo sikumbuki kwa usawia ni wapi niliiona kama ni kwenye nembo ya mgahawa huu au lile lundo la makaratasi nililonalo hotelini kwangu. Lakini akili yangu ilikuwa ina uhakika kwa asilimia kubwa sana kwamba kuna mahala nimeona mchoro wa kofia ya kifalme ya kale, kuna picha ina huo mchoro wa crown, haijalishi kama ni kwenye nembo ya mgahawa huu hapo nje au kwenye lundo la makaratasi niliyoyaacha hotelini, ninachokumbuka ni kwamba kuna mahali nimeona huo mchoro wa kofia ya kale ya kifalme.



    Kwa haraka akili yangu ikahisi imeng'amua kwamba kwa namna fulani watu hawa wameamua kumuita mtu au wameamua kuweka fumbo la mawasiliano kwa jina la 'Melchizedek' kwa kuakisi 'Melchizedek' Mfalme wa ambaye hadithi yake niliisoma miaka mingi iliyopita nikiwa sekondari katika somo la biblia kwamba kwamba Mfalme huyo wa kusadikika alimtokea Ibrahim na kumbariki. 'Melchizedek' huyo huyo mahala mwingine kwenye hadithi za biblia anaitwa kuwa ndiye kuhani mkuu huko mbinguni.



    Kwa namna fulani nikaanza kujihisi labda nilikuwa naanza kuchanganyikiwa kwa kuhusisha masuala ya biblia na changamoto na kitendawili kilichopo mbele yangu.

    Lakini bado upande mwingine wa akili yangu ulikuwa unaniambia kwamba niko sahihi na uwendawazimu wangu. Nikajikuta najiuliza kama niko sahihi, huyo Melchizedek ndivyo vivyo wanavyomaanisha, je fumbo hili lina kipande gani ambacho napaswa kukijua??

    Nikajijibu mwenyewe, kwamba kwa mujibu wa hadithi hizo nilizosoma huko sekondari ni kwamba Melchizedek ndiye kuhani mkuu pekee huyo mbinguni ambaye anaweza kuingia mahala patakatifu pa hekalu.





    Nikahisi nimepata jawabu la fumbo hili ambalo lilikuwa nahisi natakiwa kulitengua. Sidhani kama nimewahi kuhisi kwamba mimerukwa na akili kama sekunde hizi kumi za maisha yangu. Kwanza kabisa sikuwa na hakika kama ni kweli swali hili la "where is the package?" Mzee huyu alikuwa anauliza kama fumbo au kulikuwa na mzigo kweli ambao alikuwa anautegemea kutoka kwa 'Melchizedek'? Lakini akili yangu ikanipa moyo kwamba hilo lilikuwa ni fumbo.

    Lakini pili lilikuwa ni jibu la hilo fumbo, hakuna namna ambayo naweza kubuni jibu la fumbo la watu kuwasiliana kwa siri alafu niwe sahihi, lilikuwa ni kama vile nipatie namba ya siri ya mtu ya kufunga simu yake au labda namba yake ya siri ya kadi yake ya benki, hakuna namna ambayo naweza kutoa jawabu sahihi la fumbo hili la wao kutaka kunithibitisha kama kweli nimetumwa na Melchizedek. Lakini nikajipa moyo, kile nilichokifikiri ndani ya sekunde hizi kumi ndicho hicho ambacho nitakijibu.



    Nikalirudia tena kichwani lile swali aliloniuliza yule mzee, "Where is the package?"



    Nikavuta pumzi na kuishusha, kisha kwa kujiamini nikamuangalia machoni na kumjibu,



    "The package is at the holly place.!!"



    Sikumbuki kwa usahihi zaidi ni kwa muda gani alinitazama machoni bila kupepesa, lakini ilikuwa ni zaidi ya dakika moja tulikaziana macho baada ya kutoa jawabu langu hili.

    Japokuwa usoni nilikuwa nimekaza macho na kuonyesha kujiamini lakini moyo ulikuwa unanienda mbio kama nimekimbia marathoni ya kilomita mia. Kijasho chembamba kilikuwa kinanivuja ndani ya nguo.



    Baada ya kama dakika nzima ya kutazamana kwa kukaziana macho hatimaye nilimuona yule mzee anatikisa kichwa katika namna ya kuitikia, yaani kukubali. Maana yake kwamba nimetoa jawabu sahihi.!!!



    "what the fuuuccckk!!" nilijikuta najitamkia mwenyewe kichwani mwangu kimya kimya. Nilihisi kama vile naota… kilichotokea ni kitu ambacho hata mtu ninaye muamini angenisimulia nisingeamini!! Inawezekanaje???

    Nimepambana na The Board na kuwadondosha, nimeunda moja ya taasisi bora zaidi nchini Kwetu Tanzania, lakini hakuna siku ambayo nilijitukuza mwenyewe na kukubali jina la 'kichwa' kama siku hii ya leo. Nilihisi kama vile nastahili kutunukiwa tuzo ya Nobel au labda jina langu kuandikwa sambamba na majina ya akina Albert Einstein, Newton, Galileo na wanaofanana nao.

    Nilijitahidi nisionyeshe mshangao wangu usoni… uzuri mapigo ya moyo yalirudi kuwa kawaida na kijasho kilichokuwa kinanitoka awali kilikauka.



    "Go back to your hotel and wait.!"

    Yule mzee wa kichina akaongea.



    "What.!?" Nikamuuliza nikiwa kama nimezinduka kutoka usingizini.



    "I said go back to your hotel and wait…. ##-@+@%$-$+#&@-&@%@-@%@"



    Yule mzee akaongea huku akimalizia na kichina anamuambia yule kijana ambaye alinileta huku juu akiwa amenikwida kutoka 'floor' ya chini.



    Nilitamani nimuulize yule mzee "wait for what?" Lakini nilihisi kwamba nikiuliza tu swali hilo wanaweza kung'amua kwamba sijatumwa hapa na Melchizedek na wala nilikuwa sijui ninachokifanya.

    Kwa hiyo sikuongea chochote nikaanza zangu kuondoka huku yule kijana aliyenileta akinifuata kwa nyuma. Nilielewa kuwa yule mzee alimuamuru 'aniescort' mpaka nje ya jengo nisije kuwafanyia uhuni fulani labda.



    Nikashuka mpaka chini nikiwa nasindikizwa na yule kijana, akanifungulia ule mlango wa nyuma wa jikoni kisha nikatembra na uchochoro mpaka kutokea barabarani mbele ya jengo la huu mgahawa.



    Kitu cha kwanza tu nilipofika mbele ya jengo nikaangalia 'logo' ya mgahawa na yale maandishi yake ya kichina. Katika nembo pale kulikuwa na mchoro fulani hivi uliorembwa wa Kofia ya kifalme ya kale.

    Nikajikuta natabasamu peke yangu kwa sababu tangu siku ya kwanza naona mgahawa huu sikuwahi kuhisi au kutilia maanani nembo hii kiasi cha kujua kulikuwa na mchoro huo wa Kofia ya kifalme lakini ajabu ni kwamba ubongo wangu ulihifadhi sawia mchoro huo na kuniletea hiyo kumbukumbu pale nilipohisi kuhitaji.



    Japokuwa nilitabasamu kutokana na kujinasua kwenye mtego, lakini kichwani maswali yalizidi maradufu! Melchizedek ni kitu gani hasa? Yule mzee ameniambia nirudi hotelini na kusubiri, nasubiri nini? Ni nini hasa kinaendelea??

    Kwa kiwango fulani nikaanza kujutia uamuzi wangu wa kuja hapa Zurich, lakini nilijutia zaidi uamuzi wangu wa kufungua bahasha ambayo nilipewa na marehemu baba yangu… nikajikuta naanza kuwaza Cheupe ana hali gani nyumbani Tanzania, vipi kuhusu mwanangu?

    Japokuwa hatukuwa na maelewano mazuri na Cheupe mpaka siku naondoka Tanzania, lakini nilijikuta natamani angekuwa hapa usiku huu… nilitamani kama nirejeapo hotelini nimkute! Anikumbatie nilale kama mtoto mchanga na kunifarini kuwa kila kitu kitakuwa sawa… nilijikuta natamani nipae na kutua Tanzania na kumwambia nampenda mkewangu licha ya sintofahmu ya mahusiabo yetu. Nikakata shauri kwamba nikirejea tu hotelini nimpigie simu kabla ya kufanya lllotr lile.



    Nikatembea kurejea hotelini huku nimeinamisha kichwa nikiwaza na kuwazua juu ya kila kinachoendelea katika maisha yangu.





    Kutoka na kutembea taratibu nikitafakari nilitumia karibia dakika arobaini nzima kufika hotelini kwangu. Nilipofika tu mlangoni na kuingiza funguo kwenye tundu lake nikaisikia ile hali ambayo niliisikia awali kabla sijaondoka, kwamba siko peke yangu. Mwili ulikuwa unanisisimuka nikihisi kama vile kulikuwa na mtu mwingine ndani ya chumba changu. Vinyweleo vilisimama na mwili ulikuwa unasisimuka kama chaji ya umeme inapita.



    Nikafungua mlango taratibu na kuingia ndani. Nilipoingia tu mara moja puani nikaanza kusikia harufu fulani hivi hafifu. Kama harufu ya kemikali au labda manukati ya bei chee.





    Harufu fulani hivi ambayo nilikuwa naijua lakini nilishindwa kukumbuka sawia ni harufu ya nini. Nikageuka na kutazama huku na huko nione labda naweza kupata jawabu lakini wapi. Niakingia chumbani, nako kulikuwa na hiyo harufu ya kemikali au manukato ya bei ya chini lakini kila kitu kilikuwa vile vile kama ambavyo nilikiacha. Nikapekuwa mkoba nilioweka makabrasha na makaratasi yangu, yalikuwa vile vile kama ambavyo niliacha.

    Nikarejea tena sebuleni, hakukuwa na mabadiliko yoyote tofauti.



    Nikaelekea bafuni… nilipoingia tu moja kwa moja macho yangu yalitua kwenye 'sink' la kunawia uso na kupiga mswaki… kila kitu kilikuwa sawa kasoro kitu kimoja tu ambacho kilinifanya ning'amue hii harufu ilikuwa ni harufu ya nini! Miswaki ilikuwepo sawa kabisa, dawa ya meno, dawa ya kunyolea ndevu na sabuni.! Lakini pamoja na hivi kulikuwa na kikopo cha 'WINDEX'. Maji maji (kemikali) ya kusafisha madirisha na milango na meza za vioo. Kikopo kilikuwa kwenye mtindo wake ule ule ambavyo vibatengenezwa na mbele kuna kimshikio ambacho ukiminya vimaji maji vinaruka.



    Nikajiuliza tena na tena, hiki kikopo kilikuwa hapa kabla sijaondoka?? Jibu nikawa sipati kwa sababu ni suala ambalo sikutilia maanani awali… lakini swali lingine linanijia kuwa harufu hii ninayosikia ni ya hii Windex kwa maana kwamba muda mchache uliopita imetumia kusafisha vitu humu chumbani, nikajiuliza kama hilo suala linawezekana, chumba cha Hoteli kusagishwa usiku huu bila mimi kuomba? Na nilishangaa kwa nini harufu iwe kila mahala, kama ingetumia kusafisha vioo vya madirisha tu nisingeweza kuisikia… lakini pia kwa nini hiki kikopo kiachwe hapa? Kwa ninavyojua wakimaliza usafi lazima waondoke nacho kusafisha vyumba vingine!!!



    Mwili ukaanza kunisisimuka nikihisi kabisa hapa kuna jambo haliko sawa.



    Nikakibeba kile kikopo kwa haraka na kwenda nacho mpaka chini mapokezi…



    "You guys forgot this in my room!" Nikamuambia yule binti wa mapokezi huku natabasamu.



    "What do you mean?" Akaniuliza kwa mshangao.



    "I found this inside my room so I assume its yours…" nikaongea tena huku natabasamu.



    "No its not ours?" Yule binti akanijibu kwa kujiamini.



    "What? What do you mean?" Nikauliza kwa mshangao.



    "First we don't use that brand… we use 'Glass Plus'… and second its not likely for us to forget it in your room and if so we would have came and picked it up since afternoon!"



    "I assumed may be you guys forgot it this evening!"



    "No way! We only do the cleaning in the morning unless requested by the customer!"



    Nikabaki namuangalia tu huku nahema juu juu. Kuna kitu nilianza kuking'amua kichwani na sikukipenda. Kiliniogopesha.!!



    "Sir is everything OK?" Yule binti akaniuliza kwa udadisi.



    "I am perfect! Thank you!!"



    Nikamjibu huku naondoka kwa kasi bila kuangalia nyuma. Moyo nilikuwa nausikia unadunda kama vile unataka kutoka. Niliogopa mpaka miguu ikawa inagongana nikitembea. Nilielewa ni nini kimetokea chumbani kwangu. Na kwa nini harufu hiyi ilitawala chumbani kwangu kila mahala.

    Kutokana na mapambano yangu na The Board mwaka mmoja uliopita yalinipa uzoefu wa kujua mambo mengi ambayo watu wengi hawayajua. Nilielewa nini kimetokea kwenye chumba changu cha hotel na kila nilivyozidi kuunganisha nukta nilitamani nipae nipotee au ardhi ipasuke nisionekane.



    Kemikali ya kusafisha vioo (glass cleaner) ndio njia bora zaidi ya kufuta alama za vidole kwenye kitu chochote. Ukifanya tukio lolote na hutaki kubakisha alama za vidole ili usije kubainika basi tumia glass cleaner kufuta kila mahala ulikoshika.

    Hii ilimaanisha kwamba muda mchache kabla sijarejea hapa hotelini kuna kitu kimefanyika chumbani kwangu na baada ya kitu hiki kufanyika walioyekeleza wamefuta alama zao za vidole.!!



    "What the **** is going on here?"



    Niliongea kwa sauti kubwa na kwa hasiri huku natetemeka ma kuvuja jasho.



    Kichwani nilikuwa na lundo la maswali ambayo hayana majibu na sasa nilianza kuhisi hatari juu ya maisha yangu mimi mwenyewe.!!







    Nilikuwa bado nimesimama katikati ya chumba changu cha hoteli nikitazama na kujaribu kufikiri. Bado nilikuwa naisikia ile harufu ya windex kwa mbali sana puani kwangu. Nilijiuliza kama huyu mtu ambaye aliingia chumbani kwangu humu na kufanya kile ambacho alikifanya na kisha kufuta alama zake za vidole kwa sababu ambayo sijaijua mpaka sasa, nilijiuliza hilo kopo la hii windex alisahau kwa makusudi au bahati mbaya. Kuna nini kilikuwa kinaendelea? Safari yangu ya kuja hapa Zurich imekuja kunichanganya zaidi akili na kuniacha na maswali mengi kuliko majibu. Nilidhani uwepo wangu hapa Zurich ungelisaidia kunitoa gizani rohoni mwangu, giza ambalo limekaa nafsini mwangu kwa takribani mwaka mzima tangu siku ambayo baba yangu alijipiga risasi mbele yangu. Lakini safari yangu hapa Zurich kwa sasa nilihisi imeniingizia giza zaidi nafsini badala ya mwanga niliokuwa nautarajia.



    Niligeuka tena huku na huko pale chumbani. Kichwani sikuwa napata jawabu lolote la nini hasa kilikiwa kinaendelea. Kitu pekee nilichokuwa nakihisi ni ukimya. Kwa mara ya kwanza nikahisi labda ukimya huu ninao hisi kila mara hauko kwenye chumba hiki bali upo nafsini mwangu. Ukimya wa upweke na ukimya wa kujihisi kupotea.



    Nikaitazama simu yangu niliyoiweka juu ya meza pale katikati ya sebule, niliitazama kwa sekunde kadhaa nikitamani walau ilie na juu yake kwenye kioo nione namba kutoka Tanzania, namba ya mkewangu Cheupe. Lakini zilikuwa zimepita siku kadhaa bila kuona simu ya Cheupe na mimi sikujua ni kitu gani ambacho kilikuwa nafsini mwangu lakini nilishindwa kuinua simu na kumpigia.



    Nikafumba macho kwa nguvu huku nikiinua viganja vya mikono na kujifunikanavyo usoni. Ilikuwa kana kwamba ulimwengu wangu wote unadondoka mbele yangu huku nikiutazama nisijue ni nini cha kufanya.



    Kuna muda mtu unatamani labda ungeliweza kuandika namna gani unataka maisha yako yawe. Unatamani uandike kama riwaya tamu kuhusu maisha yako na hayo ndio yawe maisha yako halisi. Upweke ambao uko nao nafsini ujazwe na kufunguka na nyuso za tabasamu. Hofu ulizo nazo zigeuke kuwa uimara wa kuitafuta kesho nyingine yenye furaha zaidi. Kiza ambacho kimeijaza nafsi yako ukiondoe kwa nyakati murua za nuru.

    Unatamani uwe mwandishi mahiri wa riwaya halisi ya maisha yako. Unatamani kila kitu kiwe sawia vile ambavyo unaota usiku.



    Lakini hatukujaliwa karama hii ya kuandika maisha yetu tunataka yaweje, tumepewa maisha ambayo hatukuyachagua. Hatuwezi kuchagua maumivu gani tuyapitie katika maisha. Hatuwezi kuchagua mateso, hatuwezi kuchagua mafarakano, hatuwezi kuchagua taharuki, hatuwezi kuchagua machozi, na wala hatuwezi kuchagua moyo mgumu. Na ndio maana katika nyakati za fadhaa kama siku hii ya leo kila siku usiku ni swali moja tu tunajiuliza kichwani, kwa nini? Kwa nini hatukujaliwa karama ya kuwa waandishi wa maisha yetu tuyatakayo.



    Ukiwa katika fadhaa namna hii kuna muda unashindwa kuona uhalisia, uhalisia wa kwamba maumivu haya ndio ambayo yanafanya furaha ya kesho iwe na ladha tamu na nzuri zaidi. Maumivu haya yakishapita na kuona ni namna gani maisha yanaweza kuwa sio kumbukumbu ya yalikuwaje, ndipo hapa ambapo unageuka nyuma na kukumbuka siku hizi za fadhaa, siku hizi za upweke, siku hizi za kujihisi umepotea na kumshukuru Mungu kwa sababu bila maumivu haya ya leo usingeweza kuona utamu wa furaha ya kesho na uimara wa moyo wako.



    Nikageuka tena huku na huko kutazama sebule na chumba hiki cha hoteli. Bado nilikiwa nahisi ule ukimya, bado puani nilikuwa nasikia harufu ya ile windex ya kusafishia vioo vya madirisha. "Go back yo your hotel and wait", nikakumbuka kauli ya mwisho ya yule mzee wa kichina.



    "Wait for what.!?"



    Nikajikuta nang'aka peke yangu kwa hasira. Tangu nimefika hapa Zurich imekuwa ni mfululizo tu wa kupokea amri na maagizo nisiyoyaelewa ambayo yananichanganya akili siku baada ya siku. Mara ya kwanza nilipewa maelekezo ya kwenda kwenye lile jengo la HARDSTRASSE 201, 1985. Huko nako nikakutana na ujumbe wa kurekodi wa marehemu baba yangu ambao ulinifikisha mpaka kwa kikundi cha Hudini. Kule nako nimepewa lundo la nyaraka bila maelezo yoyote yale. Na hata baada ya kung'amua japo ukweli mdogo kwenye zile nyaraka na kisha kufika kwenye ule mgahawa wa kichina bado huko nako napewa maagizo ambayo siyaelewi. Ati "go back to your hotel and wait.!?"



    "Wait for what??" Nikang'aka tena huku nikiinuka kutoka kwenye sofa na kuanza kutembea pale sebuleni kwa hasira.



    "Wait for what?" Nikaongea kwa hasira zaidi nikitembea kutoka upande mmoja wa sebule mpaka mwingine na kurudi tena.



    Kichwani mwangu nikaanza kujewa na hisia kwamba kama nitaendelea kufuata maelezo haya ambayo siyaelewi na kwa kiaisi fulani nikiyaona kama hayanisaidii ninaweza kukaa hata mwaka mzima hapa Zurich na nisifanikishe chochote kile. Nikaanza kujewa na hisia pia kwamba labda inawezekana watu hawa wanataka kunitumia ili kufanikisha lengo lao fulani ambalo labda wanashindwa kulifanikisha bila mimi. Kwa sababu inawezekanaje nipewe lundo la nyaraka pamoja na picha alafu anayenipa anadai kwamba hajui chochote kile kuhusu nyaraka hizo au picha hizo.

    http://pseudepigraphas.blogspot.com/

    Nikaanza kuvuta kumbukumbu ya zaidi ya mwaka mmoja uliopita, namna ambavyo nilipambana na kuidondosha jumuiya ya siri ya The Board mimi mwenyewe pekee. Moyoni nikaanza kujawa na ushujaa, kama niliweza kufanya vile kipindi kile nawezaje kushindwa kufanya hivyo sasa?



    "Nimekuja Zurich kutafuta majibu sio kupata vitendawili zaidi… am done taking orders from anyone!"



    Nikatembea kwa hasira mpaka chumbani na kuanza kutoa mabegi yangu ya safari kutoka kwenye kabati. Nikapanga vitu vizuri pamoja na lile lundo za nyaraka nilizozitoa kule kwenye nyumba ya baba yangu au yangu kama nilivyoelezwa pamoja na nyaraka ambazo nilipewa na Hudini.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog