Search This Blog

Friday 18 November 2022

FUMBO LA UTAMBUZI - 5

 





    Simulizi : Fumbo La Utambuzi

    Sehemu Ya Tano (5)





    Koplo Mbegu alishangaa ameshikwa mkono anazidi kuingizwa gizani tu na mtu asiyemjua, lakini moyoni alikuwa anamshukuru mtu huyo kumuokoa kutoka kwenye tundu la mauti, maana tayari alikuwa ameshakubaliana na matokeo ila wakati anataka kufyatuliwa tu risasi alishangaa taa zimezimwa kisha akavutwa kwa nguvu na kutolewa nje na kuingizwa gizani na kuanza kukimbia huku ameshikwa mkono bila kumjua huyo mtu aliyemuokoa.



    Walizidi kukimbia tu, mwisho yule mtu alimuachia mkono Koplo Mbegu na akasimama kisha akamgeukia Koplo Mbegu, alikuwa ni Sudi Bakari, Koplo Mbegu akahamaki,.



    "Upo chini ya ulinzi kwa kuhusika na mauaji ya viongozi wa nchi" Koplo Mbegu aliongea huku akimfuata Sudi Bakari,



    "Kiumbe usiye na shukrani unatakiwa unishukuru, nimekutoa kwenye taswira ya umauti lakini bado unataka kuniweka hatiani?" Sudi Bakari aliuliza huku akimuangalia Koplo Mbegu,



    "Nafuata sheria, upo chini ya ulinzi" Koplo Mbegu aliongea,



    "Sheria unayoifuata ndiyo iliyotaka kukuletea umauti" Sudi Bakari alijibu huku akianza kuondoka,



    "Hutii sheria sio?" Koplo aliongea huku akimfuata lakini Sudi Bakari aliendelea kuondoka tu, Koplo Mbegu akaona analetewa dharau, aliongeza kasi ya kutembea na alipomfikia alinyanyua mkono kwa ajili ya kumpiga Kofi Sudi Bakari, mkono wa Koplo Mbegu ulilenga sawia usawa wa shingo ya Sudi Bakari lakini ule mkono ukapita kama kapiga kofi upepo vile, Koplo Mbegu akabaki anashangaa, lakini hakukoma, alidhamiria kumtia kizuizini Sudi Bakari.



    Sasa Koplo Mbegu aliamua kutumia nguvu, aliamua kumpiga ngwala Sudi Bakari, wakati Koplo Mbegu akivuta mguu wake kuelekea kwenye miguu ya Sudi Bakari, Sudi Bakari aliudaka mguu wa Koplo Mbegu kisha Sudi Bakari akaachia ngumi ya wastani iliyopiga unyayo wa chini wa Koplo Mbegu na hapo Koplo Mbegu akahisi kama amepigwa na shoti ya umeme, Sudi Bakari akauachia mguu wa Koplo Mbegu kisha akaanza kuondoka, hata Koplo Mbegu alipojaribu kumfuata alishindwa, mguu wake ulikuwa umejaa ganzi kiasi kwamba hata kutembea alikuwa hawezi.



    Sudi Bakari alipopotea machoni kwa Koplo Mbegu, ndipo Koplo Mbegu alihisi ganzi kumuachia, akaweza kunyanyuka na kuelekea kwenye njia aliyoelekea Sudi Bakari lakini hakuweza kumuona tena.



    Koplo Mbegu akaamua kuitafuta barabara ya kumrudisha kwake, wakati akiwa anaelekea kwake ndipo alipoiona gari nyeusi ikija na Barabara ile ile, akajificha pembezoni mwa ukuta, hakutaka kumuamini mtu, ile gari ikapita, kitu ambacho Koplo Mbegu hakukijua kuhusu ile gari ni kuwa lile gari ndilo walikuwepo Gabby na Jimmy na muda huo walikuwa wanaondoka baada ya kushindwa kutimiza hadhma yao.



    Koplo Mbegu alitoka mafichoni na kuendelea kutembea kwa tahadhari kuelekea kwake huku akiwa makini na kila mtu anaepishana nae usiku huo na ukizingatia alikuwa na bukta tu bila kuwa na kitu juu, kwa maana hiyo alikuwa kifua wazi na pia alikuwa pekupeku, yaani miguuni hakuwa na kiatu wala soksi.



    Alifika nje ya nyumba yao na kuanza kuchunguza kwa mbali kama kunauwezekano wa watu wabaya kuwepo chumbani kwake.



    Wakati akiwa bado anaangalia kwa mbali aliweza kumuona jirani yake mmoja akimgongea mlango, Koplo Mbegu akaamua aende,



    "Vipi?" Koplo Mbegu alimuuliza kwa nyuma na kumfanya jirani yake ashtuke na kugeuka nyuma kwa uoga,



    "Niazime pasi ndugu yangu" Jirani aliongea kwa tabasamu baada ya kumgundua Koplo Mbegu,



    "Ingia tu jirani uchukue, ipo chini ya meza ya runinga" Koplo Mbegu aliongea ili jirani yake aingie ili yeye ajue Kama bado wale wabaya wako ndani.



    Baada ya dakika moja jirani alitoka ndani huku akiwa na pasi mkononi,



    "Umeiona ee?" Koplo Mbegu alimuuliza huku akijifanya anafanya mazoezi ya kuruka kichura chura,



    "Nimeiona jirani, nairudisha muda si mrefu" Jirani aliongea huku akielekea kwenye chumba chake,



    "Sawa jirani" Koplo Mbegu aliongea huku akiingia chumbani kwake baada ya kujiridhisha na usalama.



    Aliingia na kukagua kwa macho, akaona pako salama isipokuwa kwenye eneo la kitanda kulikuwa na matundu juu ya godoro, Koplo Mbegu akachungulia chini ya kitanda na kuona yale matundu yametoboa mpaka ardhi, akajiridhisha kuwa yale matunda ni ya risasi.



    Akachukua simu yake na kuitafuta namba anayoitaka na kupiga.



    ******************



    Tom baada ya kuhama ile nyumba aliyokuwa anakaa hawali, alisafirisha vyombo vyake kwenda morogoro kwa wazazi wake na yeye alitafuta gesti moja eneo moja lililojificha sana na ilikuwa ngumu sana mtu yoyote anaemjua kufika eneo hilo.



    Sehemu ya mapokezi ya hiyo gesti kulilikuwa na eneo ambalo liliwekwa viti na mbele ya hivyo viti paliwekwa runinga kubwa ya kisasa ilikuwa imebandikwa ukutani, siku hizi mnaziita flat screen.



    Palikuwa na watu watatu wakiangalia marudio ya habari usiku ule wa saa sita, na mmoja kati ya vijana hao alikuwa ni Tom ambaye alivaa jaketi kubwa na kofia ya kapelo, alikuwa anasubiri ile habari iishe ili akalale ndani ya chumba chake ambacho siku hiyo runinga ya chumbani kwake ilikuwa na itilafu kwa hiyo ilimbidi kujumuika hapo na wafanyakazi kadhaa wa hiyo lodge.



    Wakati Tom akiendelea kutazama runinga, mlango mkubwa wa kuingilia ndani ulisukumwa na akaingia Koplo Mbegu, Koplo Mbegu alipoingia tu akaanza kuzungusha macho ndani ya eneo hilo............



    Koplo Mbegu aliangaza macho kushoto na kulia na mwisho akaona anapopahitaji, akaanza kupiga hatua kuelekea mapokezi huku mkononi akiwa na begi dogo.



    Alitembea mpaka kwenye dirisha la mapokezi na kumsalimia dada wa mapokezi,



    "Naweza kupata chumba?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Vyumba vipo" Dada wa mapokezi alijibu,



    "Nahitaji kimoja" Koplo Mbegu aliongea,



    "Elfu thelathini kwa siku" Dada wa mapokezi alijibu,



    "Sawa, nipeleke upo chumbani" Koplo Mbegu alijibu,



    "Lipia kwanza, alafu utapatiwa chumba chako kaka" Dada wa mapokezi aliongea na kisha Koplo Mbegu akalipia chumba alafu akapelekwa mpaka ndani ya chumba chake,



    "Alafu nilisahau kukuandika jina na pia uwa tunakagua mizigo ya kila Mteja wetu" Dada wa mapokezi aliongea baada ya kufika ndani ya chumba,



    "Kagua" Koplo Mbegu akaongea huku akifungua zipu ya begi lake na kumwaga kitandani vitu vyote vilivyopo ndani ya begi na Dada wa mapokezi akaanza kukagua, ila alishtuka alipoziona pingu,



    "Usiogope" Koplo Mbegu aliongea huku akimuonesha kitambulisho chake,



    "Kumbe ni polisi? haya nipe jina lako nikaandike" Dada wa mapokezi aliongea,



    "Naitwa Said Mbegu, au nenda na kitambulisho ukishamaliza kunakiri utanirudishia" Koplo Mbegu aliongea huku akianza kuzirudisha nguo zake ndani ya begi,



    "Ni jambo zuri" Dada wa mapokezi aliongea kisha akakinyakua kitambulisho cha Koplo Mbegu na kutoka nacho nje.



    Koplo Mbegu alipomaliza kuzirudushia nguo zake, alilitupia begi kwenye kochi lililopo hapo chumbani, kisha lililomtokea yake na kujitupa kitandani na kuanza kutafakari tukio lililomtokea.



    Baada ya muda alisikia mtu akigonga mlango wa chumba alichofikia, Koplo Mbegu akamruhusu aingie, akaingia, alikuwa ni yule dada wa mapokezi alikuwa amerejesha kitambulisho cha Koplo Mbegu,



    "Kiweke hapo mezani" Koplo Mbegu aliongea huku akimtupia jicho yule mwanadada,



    "Kama unataka kinywaji utachukua hapo kwenye friji" Dada wa mapokezi aliongea huku akioneshea kidole friji iliyopo kwenye pembe ya chumba,



    "Oooh kumbe kuna friji, asante kwa kunihabarisha" Koplo Mbegu aliongea huku akitabasamu,



    "Usiku mwema" Dada wa mapokezi aliongea kisha akatoka na kuurudishia mlango na kumuacha Koplo Mbegu akimtazama kwa jicho la wizi.



    Baada ya dakika tano akachukua simu yake na kumpigia mkuu wake, hii simu ni mpya kabisa na hata line ilikuwa mpya kabisa alivitoa ndani ya kabati la chumbani kwake kwa kuwa vilikuwepogi tu. Aliamua kubadilisha simu na line kwa sababu zake za kiusalama kwa maana alijua kabisa njia kubwa wanayotumiaga usalama wa taifa katika kumtafuta mtu njia kubwa ni katika kufuatilia mawasiliano ya mtu wanayemtafuta.



    Baada ya kutoa line mpya aliongeza salio na kumpigia mkuu wake na kisha akamueleza kila kitu kilichomtokea usiku huo, na zaidi alimwambia kuwa hata kwake amehama kwa muda kwa kuhofia kuuawa na watu hao ambao alidai ni wafanyakazi wa usalama wa taifa, mkubwa wake akataka kesho asubuhi waonane ili kuzungumza zaidi, baada ya hapo Koplo Mbegu alikata simu na kunyanyuka kuelekea kwenye friji na kuangalia ni vinywaji gani vilivyopo, akakuta maji mawili makubwa, bia mbili na soda tatu, akachukua maji na kurudi nayo kitandani, akayafungua kisha akayagida mafundo kadhaa na kuishusha chupa chini, akazima taa na kulala.



    *****************



    Jimmy na Gabby walirudi ndani ya kambi yako huku wakionekana hawana furaha kabisa. Gabby alipofika alipitiliza chumbani kwake na Jimmy aliishia sebuleni na kujitupa pembeni ya kochi jirani na BQ,



    "Mbona mnaonekana hamna furaha? au tayari mmeshamkosa hata huyo afande?" BQ aliuliza huku akimtupia jicho Jimmy,



    "Kweli tumemkosa, inaelekea hayupo kwa maana tumemsubiri sana nje ya nyumba na hatujaona akirudi, na hata tulipoingia ndani hatukumuona" Jimmy alijibu,



    "Sasa mbona mpaka dakika hii simu yangu inaonesha kuwa line ya simu ya huyo Jamaa ipo maeneo yale yale ya mtaani kwao?" BQ aliongea huku akimuonesha Jimmy simu yake,



    "Ebu mpigie?" Jimmy aliongea na BQ akajaribu kupiga ila siku iliita bila kupokelewa,



    "Labda amelala" BQ alijibu wakati simu ikijikata yenyewe,



    "Labda simu ameiacha chumbani alafu yeye ametoka, maana tumetoka sasa hivi tu" Jimmy aliongea,



    "Itabidi kesho niende mimi mweyewe, maana nyie kama hampo serious vile" BQ aliongea,



    "Usiseme hivyo BQ, kwanini tusiwe serious wakati huyu mtu ni hatari kwetu sote?" Jimmy aliuliza,



    "Basi kesho nitaenda mimi ili kazi iwe rahisi zaidi" BQ aliongea,



    "Sawa. Waziri yupo wapi?" Jimmy aliuliza,



    "Alienda kulala" BQ alijibu,



    "Basi poa, acha na mimi nikalale" Jimmy aliongea,



    "Poa, mimi naondoka, nitarudi kesho" BQ aliongea huku akiinuka. Huyu mwadada uwa halali hapa, anaishi kwake.



    BQ alitoka na kuchukua gari yake kisha akaelekea kwake.



    Jimmy alifunga mlango na kuelekea chumbani kwa Gabby,



    "BQ anasemaje?" Gabby alimuuliza Jimmy,



    "Amesema itabidi kesho yeye ndio arudi kumuua yule askari" Jimmy alijibu,



    "Muache aende, ila nadhani yule Jamaa hawezi kurudi kwake, kwa lile tukio ni lazima pale" Gabby aliongea,



    "Ila uzuri ni kuwa simu yake tulimuachia, kwa hiyo popote atapokuwa ni lazima tupajue kutokana na mtandao" Jimmy aliongea,



    "Kwa hiyo BQ amesema atatumia njia hiyo?" Gabby aliuliza,



    "Ndiyo njia anayotumia hiyo, amejaribu kumpigia ila simu ya yule afande iliita tu bila kupokelewa" Jimmy alimwambia Gabby,



    "Ila BQ yupo makini sana na mipango yake, kama ameamua kumfuatilia huyo polisi, ni lazima amuue" Gabby aliongea,



    "Itakuwa vizuri, sasa acha mimi nikalale" Jimmy aliongea huku akiinuka,



    "Samahani naomba uniletee pombe kwenye friji ya sebuleni" Gabby alimwambia Jimmy,



    "Pombe gani?" Jimmy aliuliza,



    "Niletee yoyote tu, maana nina kiu sana" Gabby aliongea na Jimmy akanyanyuka na kwenda sebuleni kumchukulia pombe Jamaa yake huyo.



    *******************



    Asubuhi ilimkuta Tom akiwa yupo kitandani, mapema akaamka kama kawaida yake na kuelekea mariwatoni, alipomaliza kujiswafi mwili aliingia kwenye mitandao ya kijamii ili kupata habari mpya, na alifanya hivyo kwa kuwa runinga ya chumbani kwake iliondolewa na kupelekwa kwa fundi, kwa hiyo siku mbili hizo alikuwa anaingia kwenye mitandao ya kijamii au alienda eneo la mapokezi kuangalia runinga.



    Baada ya nusu saa aliamua atoke chumbani kwake ili akaangalie kifungua kinywa kama kipo tayari, huo ndio ulikuwa utaratibu wa hiyo lodge wa kila mpangaji kupatiwa maziwa na mkate kila asubuhi.



    Tom alitoka na kwenda eneo la nje ambapo ndipo kulikuwa na chumba cha jiko kwa ajili ya kuandaa kifungua kinywa hicho,



    "Jamani leo mbona mmekawia?" Tom aliwauliza wakinadada wawili ambao ndio walikuwa wapishi,



    "Umeshaamka na njaa zako, ila ndio tunamalizia kuweka maziwa kwenye chupa" Dada mmoja alijibu huku akitabasamu,



    "Na usiku muwage mnapika, maana toka nimekuja nalala na njaa" Tom aliongea,



    "Si uendage ukale hotelini au kwa mama ntilie, mbona vibanda vyao vipo jirani tu alafu vipo vingi sana" Dada yule alijibu,



    "Haya nisaidie kubeba mikate ili tukagawe vyumbani" Dada mwingine aliongea huku akimkabidhi Tom box lililojaa mikate,



    "Sasa kama mnanitumikisha hivi, itabidi mnipe mikate miwili leo" Tom aliwatania huku akicheka,



    "Hata mitatu utapata, cha muhimu ni kutusaidia tu" Dada aliongea na Tom akabeba box la mikate na Dada mwingine akabeba sinia la vikombe na mwingine akabeba chupa za maziwa, wakaingia ndani ya lodge na kuanza kupita chumba kimoja kimoja wanagonga na wakifunguliwa wanapeleka hivyo vitu mezani.



    Waliendelea hivyo hivyo mpaka walipofika katika chumba cha Koplo Mbegu, waligonga mlango na kusubiri kidogo, wakagonga tena na wakasikia hatua za mtu akija kufungua mlango, baada ya sekunde chache mlango ulifunguliwa, Tom akapigwa na butwaa...........

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Tom alipigwa na butwaa baada ya mlango kufunguliwa na mlangoni alisimama dada wa mapokezi wa ile lodge,



    "Unashangaa nini sasa?" Dada wa mapokezi alimuuliza Tom,



    "Sio yeye tu, hata mimi nashangaa" Dada mpishi nae aliongea,



    "Sasa ni kipi kinachowashangaza?" Dada wa mapokezi aliuliza,



    "Kukuta asubuhi kwenye chumba cha watu, kwani wewe ni mfanya usafi?" Dada wa mapokezi alihoji huku akitabasamu,



    "Aggy hajaja leo anaumwa, ndio kaniomba nimsaidie kufanya usafi" Dada wa mapokezi alijibu,



    "Hapo umenyoosha maelezo, haya tupishe tupeleke kifungua kinywa ndani" Dada mpishi aliongea,



    "Naona leo mmeongezeka" Dada wa mapokezi aliongea kwa utani baada ya kumuona Tom nae anashirikiana na wapishi,



    "Hapa wananilipa, sifanyi bure" Tom alijibu huku akicheka, kisha wakaingia ndani ya chumba cha Koplo Mbegu na kuweka vitu mezani kisha wakatoka nje,



    "Mwenye chumba yupo wapi?" Dada mpishi alimuuliza dada wa mapokezi,



    "Yupo anaoga" Dada wa mapokezi alijibu,



    "Mwanamke au mwanaume?" Tom aliuliza kiutani huku wakiondoka,



    "Ebu nenda bwana niache nifanye usafi" Dada wa mapokezi alijibu huku akiurudishia mlango na kuendelea kufuta sakafu ya marumaru kwa kutumia kitambaa kilichokuwa na maji. Aliendelea kufuta kwa dakika mbili na Koplo Mbegu akatoka bafuni huku akiwa na kaptula na taulo mabegani,



    "Hivi kumbe kuna mfanyakazi wa kiume humu anaejihusisha na mapishi?" Koplo aliuliza huku akitabasamu,



    "Kwanini?" Dada wa mapokezi aliuliza,



    "Si wakati naoga nimesikia ukiongea na wapishi alafu nikasikia na sauti ya kiume" Koplo Mbegu alijibu,



    "Kuna kaka mmoja amechukua chumba hapa, ni mchangamfu sana" Dada wa mapokezi alijibu,



    "Hata mimi napenda sana watu wachangamfu" Koplo Mbegu aliongea huku akivaa fulana,



    "Kwani utakuwepo muda gani hapa?" Dada wa mapokezi alimuuliza Koplo Mbegu,



    "Sijajua, ila nitakaa kaa kidogo" Koplo Mbegu alijibu,



    "Basi nitakukutanisha huyo kijana ili muwe mnapiga story wote, ni mchangamfu sana" Dada wa mapokezi aliongea,



    "Anafanya kazi wapi?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Hapa inaelekea amekuja kupumzika tu, kwa maana muda mrefu sana tunashinda nae hapa hapa" Dada wa mapokezi alijibu,



    "Sawa basi, nataka kutoka asubuhi hii, nikirudi nitakutafuta ili utuunganishe nae" Koplo Mbegu aliongea huku akimimina maziwa kwenye kikombe,



    "Unaenda wapi tena?" Dada wa mapokezi alihoji,



    "Naenda kuripoti kazini, alafu nitarudi" Koplo Mbegu alijibu huku akitabasamu,



    "Sawa" Dada wa mapokezi aliongea na kuendelea kutandika kitanda, alipomaliza aliaga na kuingia chumba kingine kufanya usafi.



    Koplo Mbegu alipomaliza kupata kifungua kinywa, alivaa jeans na shati la mikono mirefu na kapelo nyeusi, alikuwa anajiandaa kutoka ili akaonane na mkuu wake.



    Saa nne asubuhi ilimkuta Koplo Mbegu akiwa kwenye mgahawa mmoja uliojificha maeneo ya mjini, mbele yake alikuwa mkuu wa polisi akiwa na maziwa na Koplo Mbegu yeye alikuwa na juisi.



    "Una uhakika kuwa kati ya hao waliokuvamia mmoja wapo yupo usalama wa taifa?" Mkuu wa polisi alimtupia swali Koplo Mbegu,



    "Nilishawahi kumuuliza dereva wako akaniambia hivyo?" Koplo Mbegu alijibu,



    "Ebu ngoja, tuangalie" Mkuu wa polisi akatoa simu yake na kubonyeza bonyeza kwa muda, kisha zikaja picha nyingi na kumpa simu Koplo Mbegu,



    "Hizo ni picha za wafanyakazi wa usalama wa taifa, angalia kama huyo mtu utamuona hapo" Mkuu wa polisi aliongea baada ya kumpa simu Koplo Mbegu.



    Koplo Mbegu akaanza kuzipitia tarataribu, baada ya sekunde kadhaa aligota kwenye picha ya Gabby, akaikuza,



    "Huyu hapa" Koplo Mbegu aliongea huku akimrudishia mkuu wa polisi simu yake, mkuu wa polisi akaiangalia ile picha kisha akaangalia jina lililopo chini ya picha,



    "Gabriel Michael Chami" Mkuu wa polisi aliongea huku akilisoma hilo jina,



    "Sijajua sababu ya yeye kutaka kuniua, au labda ni kutokana na kukwaruzana nae ile siku ya mazishi ya rais pale kwenye viwanja vya ikulu" Koplo Mbegu aliongea,



    "Kumbe tayari mlishakwaruzana mwanzo? Tatizo lilikuwa nini?" Mkuu wa polisi aliuliza,



    "Tatizo lilikuwa ni kijana mmoja ambaye nilimshuhudia katika kifo cha Waziri mkuu, nadhani nilishakueleza" Koplo Mbegu aliongea,



    "Basi inawezekana huyo kijana yupo pamoja na huyu Gabriel" Mkuu wa polisi aliongea,



    "Sidhani, kwa maana hata siku ile pale ikulu huyu Jamaa wa usalama alimpiga sana yule kijana, inaonekana hawajuani kabisa" Koplo Mbegu alijibu,



    "Basi mi nitamfuatilia huyu Gabriel, alafu nitakupa jibu" Mkuu wa polisi aliongea,



    "Basi sawa, mimi kitaendelea na upelelezi wangu" Koplo Mbegu aliongea,



    "Basi kaendelee na mambo yako, tutawasiliana" Mkuu wa polisi aliongea na kutoa bahasha ya hela na kumtupia Koplo Mbegu katika meza, kisha akanyanyuka na kuondoka zake.



    Alipopotea machoni mwa Koplo Mbegu, na yeye Koplo Mbegu alinyanyuka na kuondoka zake.



    ******************



    Asubuhi hii ilimkuta BQ akiwa ndani ya gari lake nje ya nyumba ya anayoishi Koplo Mbegu, BQ simu ilikuwa mkononi huku akisoma mazingira ya watu wanaoingia na kutoka ndani ya nyumba ile, aliyasoma mazungira kwa muda wa saa zima na kisha akashuka taratibu huku akiwa amevaa suruali ya jeans iliyombana vema na fulana nyeusi, alitelemka na kwenda moja kwa moja kwenye mlango wa Koplo Mbegu na kuusukuma, ulionekana umefungwa, akagonga mara mbili na hakuna mtu aliyejibu, akatoa funguo ndogo na kufungua mlango, kisha akausukuma taratibu na kuingia ndani, akakuta chumba kitupu, akaitupia macho siku ndogo iliyokuwepo mezani na kuangalia namba zilizompigia Koplo Mbegu, akaikuta namba yake yeye tu, akatabasamu na kuikagua ile siku kisha akatupia pale pale mezani alipoikuta hawali.



    Kisha akawa anazungusha macho ndani ya chumba kile, macho yake yakagota kwenye maganda ya risasi mawili yaliyokuwepo sakafuni, akachuchumaa na kuyaokota kisha akayaangalia,



    "Ni lazima risasi ziwe zimetumika humu humu, na kama ni mtu amepigwa basi nione ushahidi wa damu" BQ aliongea mwenyewe kisha akainuka na kuendelea kuzungusha macho na kuyagotesha kwenye godoro ambapo kulionekana kuna matundu, akasogea na kuchunguza na kugundua risasi zimepita kwenye godoro hilo, akaondoa godoro na kupata vipande viwili vya risasi vikiwa vimejichimbia chini ya sakafu, akavichimbua na kuvibeba, akaondoka zake.



    ********************



    Koplo Mbegu alirudi katika lodge mishale ya saa tisa na nusu, alifikia kuoga, alipomaliza kuoga alirudi na kujitupa kwenye kochi, kisha akawasha runinga kwa ajili ya kuangalia mpira mchana huo, akasikia mtu akibisha hodi mlangoni mwake, akamruhusu aingie, alikuwa ni yule dada wa mapokezi,



    "Nambie, umeshakula?" Dada wa mapokezi aliuliza baada ya kuingia,



    "Tayari, vipi uliniandalia chakula?" Koplo Mbegu alimuuliza huku akitabasamu,



    "Ndio, basi acha nikale mwenyewe" Dada wa mapokezi aliongea huku akiondoka,



    "Njoo ulie hapa, maana raha ya Mpira ni kutazama wengi" Koplo Mbegu aliongea,



    "Nina kazi, au nikuitie yule kijana ukae nae, maana runinga ya chumbani kwake imeharibika" Dada wa mapokezi aliongea,



    "Muite, itakuwa vizuri aje kunipigisha story hapa" Koplo Mbegu aliongea kwa uchangamfu,



    "Ngoja nikamuangalie, maana alikuwa amelala" Dada wa mapokezi aliongea huku akitoka nje na kumuacha Koplo Mbegu akitabasamu tu.



    Dada wa mapokezi alitoka mpaka kwenye chumba cha Tom na kumgongea mlango, akaruhusiwa kuingia,



    "Amka bwana, yule kaka niliyekuambia anataka mtu wa kuongea nae, anakuita" Dada wa mapokezi alimwambia Tom,



    "Nina usingizi kinoma, mwambie nitaenda baadae" Tom aliongea huku akivuta shuka,



    "Mwanaume unalala mchana? amka ukaangalie mpira" Dada wa mapokezi aliongea,



    "Mpira wanacheza nani na nani?" Tom aliuliza kivivu huku akivuta shuka,



    "Mimi sijui bwana, we nenda kaangalie, usipoupenda si utarudi kulala?" Dada wa mapokezi aliongea,



    "Ila kweli, ngoja nikaangalie mpira" Tom aliongea na kunyanyuka huku akiwa amejifunika shuka yake na kutoka nje kuelekea kilipo chumba cha Koplo Mbegu, walipofika mlangoni, Dada wa mapokezi alibisha hodi na Koplo Mbegu akaitikia, Dada wa mapokezi akasukuma mlango na kuingia ndani,



    "Ingia basi, mbona una masihara wewe?" Dada wa mapokezi alimwambia Tom ambaye alisimama mlangoni huku akicheza mziki wa singeli uliokuwa unasikika kutoka katika simu yake ndogo aliyoishika mkononi.



    "Ndio nyimbo zangu hizi" Tom aliongea huku akibinua kiuno na kuanza kukichezesha na kumfanya yule dada wa mapokezi aangushe cheko,



    "Unanichekesha mwenzio, ingia ndani bwana" Dada wa mapokezi aliongea huku akiendelea kucheka, na Tom nae akaingia ndani.



    macho ya Koplo Mbegu yakaelekea mlangoni kumuangalia huyo kijana anayesifika kuwa mcheshi na kipindi hicho hicho pia Tom nae akamtupia macho Koplo Mbegu, hapo macho yao yakagongana...............







    Tom akarudi nyuma na kutoka nje ya mlango,



    "Vipi mbona unatoka tena?" Dada wa mapokezi alimuuliza Tom,



    "Ngoja nikatoe hili shuka mwilini, narudi" Tom aliongea na kuelekea chumbani kwake na kumuacha Koplo Mbegu akishangaa tu,



    "Sasa mbona kama amechungulia na kutoka?" Koplo Mbegu alimuuliza Dada wa mapokezi,



    "Anarudi, ameenda kurudisha shuka" Dada wa mapokezi alijibu huku akitabasamu,



    "Alafu sura yake sio ngeni kabisa machoni pangu" Koplo Mbegu aliongea,



    "Itakuwa umemuona jana, maana wakati unakuja alikuwepo pale ukumbini anatazama video" Dada wa mapokezi alijibu,



    "Labda inawezekana hivyo" Koplo Mbegu aliongea na kupuuza,



    "Basi acha nikuache, huyu Jamaa anarudi sasa hivi" Dada wa mapokezi aliongea,



    "Poa" Koplo Mbegu alijibu kisha yule Dada wa mapokezi akaondoka zake.



    Kitu kilichomchanganya Koplo Mbegu na kufanya kutomtambua Tom, ni lile shuka alilojitanda Tom, maana alijifunika mpaka kichwani na kuacha nafasi kidogo iliyoacha wazi uso wake, kwa hiyo ilimuwia vigumu Koplo Mbegu kumgundua Tom mapema ingawa alikiri hiyo sura sio ngeni machoni kwake.



    Koplo Mbegu aliendelea kumsubiri Tom ili amuulize kama amewahi kuonana nae? lakini Tom hakurudi tena, Koplo Mbegu aliendelea kusubiri kwa muda mrefu zaidi lakini Tom hakurudi, muda ukaenda zaidi mpaka Mpira aliokuwa anauangalia ukaisha na mwisho akaamua ajipumzishe kitandani kwa kusinzia kidogo, maana alihisi uchovu.



    *******************



    Tom alipoondoka chumbani kwa Koplo Mbegu alikuwa na hofu sana, alijua tayari Koplo Mbegu ameshamgundua, kwa hiyo hata alivyotoka chumbani kwa Koplo Mbegu hakuelekea chumbani kwake, alinyoosha koridoni mpaka mwisho ambayo kulikuwa na kona ya kuelekea kwenye vyoo vya jumuiya.



    Alipofika kwenye kona akawa anachungulia ili kuona kama Koplo Mbegu atatoka ila hajamuona.



    "Au nimemfananisha tu, itakuwa ni uoga wangu tu?" Tom alijiuliza huku akiendelea kuchungulia, alitumia muda mrefu kukaa pale na mwisho akaamua arudi chumbani kwake.



    "Hapa sio pa kushinda, ni bora nijihami mapema, na ikiwezekana kesho nihame mapema tu, hela niliyoilipia nitaisamehe" Tom aliongea huku akijaza nguo kwenye begi lake dogo.



    Tom alipomaliza kujaza nguo ndani ya begi, aliweka begi ndani ya kabati, kisha akafungua mlango na kuangalia kama koridoni kuna usalama, alipojiridhisha alirudishia mlango wake na kutoka nje mpaka eneo la mapokezi,



    "Umeshaonana na yule Jamaa?" Dada wa mapokezi alimuuliza Tom,



    "Bado, hivi anaitwa nani?" Tom alimuuliza Dada wa mapokezi ili ajiridhishe kama ni kweli yule aliyemuona ni Koplo Mbegu,



    "Sijui nani, nimelisahau jina lake" Dada wa mapokezi alijibu,



    "Ebu angalia kwenye kitabu cha watu waliochukua vyumba" Tom alimwambia dada wa mapokezi,



    "Lile daftari limeenda kwa bosi kwa ajili ya kuangalia hesabu kama zinaenda sawa, kwani vipi?" Dada wa mapokezi aliuliza?,



    "Hamna kitu. Basi acha mimi nitoke kidogo, nitarudi baadae" Tom aliaga na kuondoka, hakwenda mbali ila alikuwa mitaa hiyo hiyo akisoma mazingira ya pale na pia alitaka kumuangalia vizuri Koplo Mbegu kama atatoka nje ili ajue ndiyo yule anaemjua yeye au kamfananisha tu?.



    ***********************



    BQ aliingia ndani ya kambi yao huku akiwa na sura isiyokuwa ya kawaida, ingawa muda wote alikuwa anatabasamu ila halikuwa tabasamu la kawaida.



    Alipofika sebuleni aliwakuta wenzake wakipata kifungua kinywa, akawasalimia na kutupa mezani yale maganda ya risasi, Gabby na Jimmy wakashtuka, wakajua tayari mchezo walioufanya siku iliyopita umegundulika,



    "Haya maganda nimeyakuta chumbani kwa yule askari aliyekuwa anamfuatilia Tom, na pia nimezikuta na risasi pia, na bastola iliyotumika ni yako wewe Jimmy. Sasa kwanini mlitumia risasi wakati mnadai hamjamkuta huyo askari?" BQ aliuliza huku akimtazama Jimmy,



    "Kiukweli yule polisi tulimkuta, ila kuna mambo ya ghafla yalitokea na tukashindwa kumuua, yaani hatukuelewa kilichotokea" Gabby alijibu,



    "Sasa kwanini jana ulidanganya?" BQ alimuuliza Jimmy,



    "Hatukuwa na njia nyingine nzuri ya kuongea zaidi ya nilichokizungumza jana" Jimmy alijibu,



    "Sasa nikisema tuanze kudanganya kwa kila hatua tunayopiga, tutafanikisha kweli mipango yetu?" BQ aliuliza,



    "Hapana, nadhani wamekosea" Waziri wa ulinzi alijibu na kipindi hicho Jimmy alikuwa akiangalia chini,



    "Hii njia mnayoitumia ni lazima ikomeshwe" BQ aliongea huku akitabasamu,



    "Kukomeshwaje sasa? cha muhimu ni wakubali kosa na waombe msamaha" Waziri wa ulinzi aliongea,



    "Ni upumbavu kwa mtu anaefanya kazi ya kuuza roho yake kutumia uongo kwa wenzake" BQ aliongea huku akiinuka,



    "Matusi hayo, hakuna mpumbavu hapa, alichofanya Jimmy kuongea vile ni kwa sababu ya hofu ya kuonekana tumeshindwa kufanya kazi kiufanisi" Gabby aliongea,



    "Nani kawaambia uongo unajenga? ni upumbavu kutetea upumbavu na mtalipa kwa huu uongo mliotumia" BQ aliongea huku akielekea kwenye friji,



    "Kwa hiyo mimi ni mpumbavu?" Gabby aliuliza huku akimuangalia BQ aliyekuwa akitoa juisi kwenye Friji,



    "Tena mkubwa tu, na mwenzio pia" BQ alijibu na kurudi kukaa kwenye kochi,



    "Nimekuvumilia sana wewe" Gabby aliongea na kurusha kwa kasi kikombe cha udongo kuelekea kwenye uso wa BQ, BQ akakiona na wakati kikimjia, akarusha mguu wake ulioenda kukipalaza kile kikombe na kisha kile kikombe kikaenda hewani kuelekea darini na kuanza kushuka, BQ akakidaka kisha akatishia kama anataka kumpiga nacho Gabby, Gabby akayumba na BQ akatabasamu,



    "Sasa kwa akili zako za kipumbavu unadhani kama kingenipata kingenidhuru?" BQ aliuliza huku akitabasamu na wakati huo wenzao walibaki na mshangao kwa tukio alilolifanya Gabby,



    "Bado unaendelea kuniita mpumbavu?" Gabby aliuliza na kuruka juu ya meza kumfuata BQ, alipomfikia alifungua take moja la mguu wa kulia kumuelekea BQ, BQ akaliona na kubinuka sarakasi ndogo na kutua nyuma ya kochi, mguu wa Gabby ukapita tena patupu,



    "Mimi sipiganagi na mtu niliyemzidi uwezo, ni sawa na kujidumaza tu, napigana na aliyenizidi ili nipate mbinu mpya" BQ aliongea huku akitabasamu,



    "Acheni ujinga bwana, sioni sababu ya nyinyi kugombana" Waziri wa ulinzi aliongea huku akionekana ana hasira,



    "Naondoka, nitarudi kesho" BQ aliongea huku akiwa na chupa ya plastiki iliyokuwa na juisi kidogo,



    "Nenda tu, unamuaga nani?" Gabby aliuliza kwa hasira huku akiwa amesimama,



    "Kumbuka, umenipiga na kikombe na umenipiga teke lakini hayakufanikiwa, na sasa ni muda wangu mimi kurudisha pigo" BQ aliongea kisha akaigida ile juisi ndogo iliyobaki, alafu mdomo wa ile chupa ya plastiki akauvunja upande ukawa na ncha, kisha kwa kasi ya ajabu aliirusha ile chupa kumuelekea Gabby, ilikuwa inaelekea usawa wa shingo ya Gabby, Gabby alishindwa kukwepa kutokana na kasi ya ile chupa, ila ile chupa ikampita Gabby na kwenda kugonga ukutani na kuanguka.



    "Sikutaka kukuua" BQ aliongea kisha akafungua mlango na kutoka nje, Gabby akahisi maumivu upande wa pembeni wa shingo, akapeleka mkono kujishika eneo lenye maumivu, ndipo alipokutana na damu ikimtiririka,.



    "Huyu mwanamke hafai, sio wa mchezo" Gabby aliongea huku akitabasamu na pia akikiangalia kiganja chake kilicholowa damu.



    *********************



    Mishale ya saa tano usiku, Tom alikuwa anajirudisha ndani ya lodge kimachale machale, alifika mapokezi na kumsalimia dada wa mapokezi,



    "Mbona leo umechelewa?" Dada wa mapokezi aliuliza,



    "Kuna sehemu nilipita. Vipi Jamaa hajaniulizia?" Tom aliuliza huku akitaka kujua,



    "Bado amelala tokea jioni ile" Dada wa mapokezi alijibu,



    "Poa, acha nikalale" Tom aliongea na kwenda chumbani kwake.



    Dada wa mapokezi nae aliona bora akamuangalie Koplo Mbegu maana ni muda mrefu toka amelala.



    Dada wa mapokezi alienda na kugonga mlango akaruhusiwa kuingia ndani na kumkuta Koplo Mbegu akiwa ameamka,



    "Vipi? umeshakula?" Dada wa mapokezi alimuuliza Koplo Mbegu,



    "Sihisi njaa, vipi mbona yule dogo hajarudi tena muda ule?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Utamuweza yule, Tom ana mambo mengi sana" Dada wa mapokezi alijibu huku akitabasamu,



    "Tom? Thomas Anthony?" Koplo Mbegu aliuliza na wakati huo ndio akaikumbuka sura ya Tom na kuifananisha na ile aliyoiona mchana,



    "Ndio jina lake hilo? Kwani vipi?" Dada wa mapokezi aliuliza huku akipata wasiwasi,



    "Chumba kipi anaishi?" Koplo Mbegu aliuliza huku akiitoa bastola yake na kumfanya dada wa mapokezi aogope zaidi,



    "Chumba cha nne kushoto kutoka mlango wako" Dada wa mapokezi alijibu huku akitetemeka,



    "Ebu twende" Koplo aliongea huku akimvuta mkono Dada wa mapokezi na wakati huo huo bastola ilikuwa mkononi, wakatoka nje na Dada wa mapokezi akamuonesha Koplo Mbegu chumba cha Tom, Koplo Mbegu akaenda mpaka kwenye mlango wa chumba cha Tom, alipojaribu kufungua, mlango ulionekana umefungwa,



    "Hakuna ufunguo wa akiba?" Koplo aliuliza,



    "Upo" Dada wa mapokezi alijibu na kisha akaenda kuleta funguo ya hakiba, aliporejea alimpa ule ufunguo Koplo Mbegu, kisha Koplo Mbegu akafungua mlango na kuingia ndani,



    "Upo chini ya ulinzi" Koplo Mbegu aliongea huku akiingia ndani kwa pupa.................





    Lakini chumbani hawakumkuta mtu, Koplo Mbegu akaanza kupekua kila mahali ili aweze kumuona Tom lakini pia hakubahatika kumuona,



    "Si umesema ameingia sasa hivi?" Koplo Mbegu alimuuliza Dada wa mapokezi,



    "Yaani sasa hivi, hata dakika kumi hazijafika" Dada wa mapokezi alijibu,



    "Kanikimbia tena" Koplo Mbegu aliongea huku akielekea nje ya mlango,



    "Hata nguo zake sizioni" Dada wa mapokezi aliongea huku akifunga kabati lililokuwepo kwenye chumba ambacho alikuwa akihishi Tom,



    "Twende" Koplo Mbegu aliongea huku akielekea mlango wa kutokea nje, alitembea mpaka getini na kumfuata mlinzi aliyekuwa anavuta sigara pembeni ya geti,

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Babu hujamuona Tom muda huu?" Dada wa mapokezi alimuuliza mlinzi,



    "Amepita sasa hivi hapa, kwani kuna nini?" Mlinzi aliuliza,



    "Amepita ameingia ndani au ametoka nje?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Ameelekea nje, na amebeba begi dogo mgongoni" Mlinzi alijibu,



    "Amekimbia tayari" Koplo Mbegu aliongea huku akirudi ndani,



    "Eti mama, Tom amefanyaje" Mlinzi alimuuliza Dada wa mapokezi,



    "Ngoja nakuja" Dada wa mapokezi alijibu huku akimfuata Koplo Mbegu.



    Koplo Mbegu aliingia chumbani kwake na kukaa kwenye kochi,



    "Mbona sielewi elewi, Tom amefanyaje kwani" Dada wa mapokezi alimuuliza Koplo Mbegu,



    "Tom ni mharifu" Koplo Mbegu alijibu,



    "Mharifu wa nini? sijakuelewa" Dada wa mapokezi aliuliza,



    "Elewa hivyo, na mpaka sasa hapa nilipo nipo hatarini?" Koplo Mbegu aliongea,



    "Kuvipi, mbona unazidi kunichanganya?" Dada wa mapokezi aliuliza,



    "Tom anatafutwa kwa kesi za mauaji na hapa alipo alikuwa amejificha baada ya kumfuatilia sana alipokuwa anahishi mwanzo, na isitoshe kikundi chao kina mtandao mkubwa, mimi kuja kuishi hapa ni kwamba walinivamia na kutaka kuniua na ndio nikapakimbia kwangu" Koplo Mbegu aliongea,



    "Aiseee, kumbe Tom muuaji? na upole wake ule na ucheshi kumbe muuaji?" Dada wa mapokezi aliuliza huku akiwa amejishika mdomo,



    "Niamisheni chumba kwa muda huu kwa ajili ya usalama wangu, kesho itabidi nihame" Koplo Mbegu aliongea na kisha Dada wa mapokezi akaanza kufanya utaratibu wa kumuamisha chumba koplo Mbegu, baada ya saa zima utaratibu wa kumuhamisha Koplo Mbegu ulikuwa umekamilika na Koplo Mbegu alikuwa kwenye chumba kingine huku akimfikiria Tom.



    ***************_***********



    Asubuhi ya leo habari iliyokuwa kubwa ni kuhusu Tammy Semmy kushinda kwa kishindo kwenye uchaguzi wa chama chake, asilimia kubwa ya wananchi walikuwa na furaha huku wengi wakiamini kuwa Tammy Semmy ni mtu mzuri, hakuna mwananchi wa kawaida aliyedhani Tammy Semmy anaweza kuwa mmbaya.



    Wakati asilimia kubwa ya wananchi wakiwa na hiyo furaha ya ushindi wa Tammy Semmy, yeye mwenyewe muda huu hakuwa na furaha, alikuwa amekaa na waovu wenzie na muda huu Tammy Semmy alikuwa akisuluhisha ugomvi uliokuwa unatokea mara kwa mara baina ya BQ na Gabby.



    "Mimi siwezi kusema nani kati yenu amekosea, ila ninachotaka kusema ni kuhusu udanganyifu, hakuna uaminifu unaoweza kupatikana kati yetu kama udanganyifu umeanza kutuingilia" Tammy Semmy aliongea na kumeza mate,



    "Hawajawahi kufanya kazi za kimataifa hawa, wangekuwa wapo na mtu kama marehemu Ben The Rat, wangepata tabu sana" BQ aliongea,



    "Ben alikuwa simba kweli, Ben kazi ya watu kumi anaifanya peke yake, Ben hakuwa wa kawaida" Waziri wa ulinzi alichangia,



    "Jamani cha muhimu tuishi kwa amani na ukweli ndani yetu, ile safari tuliyoianza nadhani inatarajia kukamilika hivi karibuni, nimeshapita kwenye uchaguzi wa chama, uchaguzi mkuu wa nchi ni mwezi ujao, kwa hiyo kipindi hiki mshikamano kati yetu uongezeke zaidi na zaidi" Tammy Semmy aliongea,



    "Mimi nadhani sina kinyongo na mtu, sihishi kwa visasi" BQ aliongea huku akitabasamu,



    "Tufanye yameisha" Gabby nae aliongea huku akiwa na plasta shingoni baada ya kujeruhiwa na BQ siku iliyopita,



    "Kuhusu Tom nadhani akiendelea kutoonekana, ni lazima tuvujishe ile video ya mauaji ya rais au Waziri mkuu, kuhusu huyo afande mliyetaka kumuua, mtafuteni na mmuue" Tammy Semmy alizungumza,



    "Na kuhusu mimi?" Waziri wa ulinzi aliuliza,



    "Wewe sitisha kwanza mpango wa kwenda kubadilisha sura, ngoja uchaguzi mkuu ufanyike alafu tutajua cha kufanya" Tammy Semmy alijibu,



    "Sawa, nakusikiliza" Waziri wa ulinzi aliongea,



    "Alafu Black Queen bado sijajua mipango yako baada ya hapa, utabaki hapa au utarudi urusi?" Tammy Semmy alimuuliza BQ,



    "Nitaondoka, suala la kurudi nitaendea kulifikiria nikiwa uko uko urusi" BQ alijibu huku akitabasamu.



    "Sasa kazi niliyobaki nayo ni kuandaa pesa ya kutosha kwa ajili ya kuonga baadhi ya sehemu zitazoleta ugumu katika uchaguzi mkuu ujao, na kazi ya kusambaza hiyo pesa mtakuwa nayo Gabby na Jimmy" Tammy Semmy alitoa maelekezo,



    "Sawa mkuu" Jimmy alijibu,



    "Sasa mimi niwaache, kama kuna mtu anashida yoyote aniambie, ila kuhusu suala la pesa msiniambie kwa maana nikitoka hapa napitia benki kuwajazia posho zenu" Tammy Semmy aliongea na kufanya sura za vijana wake zijenge tabasamu, maana suala la pesa ni jambo zuri,



    "Ila mimi nadhani kama utakuwa na muda leo, ni vema ungeenda kwenye vikundi wa vijana wa mitaani kutoa misaada, tena ongozana na baadhi ya vyombo vya habari vile maarufu ili tukio hilo la kutoa msaada litangazwe na jina lako lizidi kupepea zaidi" Waziri wa ulinzi alitoa ushauri,



    "Hilo ni jambo jema sana, tena hata tusipoteze muda, twendeni muda huu tukakusanye vitu na kuvisambaza kwenye vituo vya yatima" Tammy Semmy aliongea kwa furaha,



    "Mimi nitabaki, au na mimi nijumuike?" Waziri wa ulinzi aliuliza,



    "Wewe utabaki hapa tu, muda wako wa kuwa huru bado haujafika" Tammy Semmy alijibu,



    "Sawa bwana, haya maisha ya kujificha ni magumu sana" Waziri wa ulinzi aliongea wakati wenzake wakinyanyuka na kuanza kujiandaa kwa ajili ya kuelekea kwenye vituo vya kutoa misaada.



    **********************



    Tom aliamua kuondoka katika ile lodge usiku uliopita, aliamua kufanya hivyo baada ya kusikia maongezi kati ya Koplo Mbegu na Dada wa mapokezi.



    Usiku huo Tom alipotoka hapo hakuwa na pesa ya kutosha kwa ajili ya kutafuta sehemu nyingine ya kulipia kwa ajili ya malazi, pesa aliyobaki nayo aliipanga kwa ajili ya chakula tu.



    Kwa hiyo usiku huo Tom alitembea mwendo mrefu kwa ajili ya kutafuta eneo la kujihifadhi, na hakutaka kulala nje ya duka au vibarazani kwenye majumba ya watu, alihofia kuporwa hata pesa yake chache aliyobaki nayo, alidhamiria kuomba kulala eneo lolote la ndani.



    Aliendelea kutembea zaidi na zaidi na kuomba kulala katika nyumba zenye mageti, alikuwa anatumia uongo wa kusema yeye ni msafiri ambaye ametoka mbali na bahati mbaya mtu ambaye alitegemea kufikia kwake amemkuta amehama na hajui alipohamia na hata namba zake za simu hana, lakini kutokana na uongo wote huo bado walinzi wa mageti waligoma kumpa hifadhi na wengi wao walimshauri akalale msikitini au akatoe taarifa kituo cha polisi, huenda anaweza kusaidiwa.



    Tom hakukata tamaa, aliendelea kutembea mpaka alipofika katika kituo kimoja cha kulelea yatima, uko napo alitoa maelezo yale yale, wakamuonea huruma na kumpa hifadhi ya kulala stoo. Pia kitu kingine kilichopelekea wamuonee huruma ni miguu ya Tom kuvimba kutokana na mwendo mrefu aliotembea, miguu yake yote ilivimba utasema inapasuka.



    Tom akapelekwa mpaka stoo kisha wakampatia shuka zito, masikini Tom wa watu akajilaza na kujifunika shuka yake, usingizi mzito ukampitia kutokana na mchoko aliokuwa nao wa kutembea umbali mrefu. Hata mbu hakuwasikia.



    Asubuhi ndani ya kituo hicho kulikuwa na shamrashamra baada ya ugeni uliofika pale kituoni, ugeni ulikuwa wa Tammy Semmy na watu wake, ugeni ulikuwa umeleta misaada kwa ajili ya watoto yatima wanaolelewa kituoni hapo.



    Tammy Semmy na watu wake walipokelewa kwa shangwe na watoto wa kituoni hapo, wakaimbiwa na kuombewa kisha wakakabidhi zawadi kwa watoto na waandishi wa habari wakawapiga picha za kutosha kwa ajili ya kumpamba Tammy Semmy katika siku inayofuata.



    "Tunashukuru sana Rais mtarajiwa, sasa tunaomba tuibebe mizigo mliyotuletea ili tuipeleke stoo" Mlezi wa kituo alimwambia Tammy Semmy,



    "Mbona sioni mbebaji hapa, nawaona watoto wadogo wadogo tu, wataweza kweli kubeba viroba vya unga?" Tammy Semmy aliuliza huku akicheka,



    "Watasaidiana tu hivyo hivyo ili mradi mizigo ifike stoo" Mlezi wa kituo alijibu huku akitabasamu,



    "Hapana bwana, unawadumaza, ngoja niwaambie vijana wangu wafanye hiyo kazi" Tammy Semmy aliongea kisha akawaagiza Jimmy na Gabby wabebe ile mizigo na waipeleke stoo.



    Gabby na Jimmy wakabeba ile mizigo na wakaanza kuipeleka stop huku wakiongozwa na mlezi wa kituo, walifika mpaka stoo na kuanza kuishusha ile mizigo na wakati huo mlezi wa kile kituo alikuwa yupo mlangoni upande wa nje,



    "Gabby mcheki mshkaji amelala anakoroma hana hata habari, unaweza kumpiga hata na mche wa sabuni na asisikie" Jimmy aliongea huku akimuangalia Tom aliyekuwa amelala na amejifunika mwili mzima mpaka usoni kiasi kwamba inakuwa ngumu kwa waovu wale kumtambua, miguu aliiacha wazi na hivi alivaa pensi basi miguu yake ilionekana namna ilivyovimba.



    "Hawa wanakuwaga walinzi, jana amekesha sasa anafidia usingizi wake wa usiku" Gabby aliongea,



    "Muangalie, ana miguu ya bia, minene hiyo" Jimmy aliongea huku akicheka baada ya kuna miguu ya Tom namna ilivyovimba,



    "Imevimba hiyo, sijui ni demu?" Gabby aliuliza,



    "Ebu mfunue umuangalie, hawezi kuhisi kitu maana usingizi alionao sio wa mchezo" Jimmy aliongea na kisha Gabby akawa anasogea eneo alilopo Tom ili afunue shuka amuangalie, Gabby alivyofika aliinama na kushika shuka...........









    "Ni mgonjwa huyo, muacheni apumzike" Mlezi wa kituo cha yatima aliongea na kufanya Gabby asitishe zoezi la kumfunua Tom aliyekuwa amelala usingizi mzito hapo chini,



    "Mgonjwa ndio alale stoo? Si angelala kwenye mabweni ya watoto?" Gabby aliuliza,



    "Kwenye mabweni kuna kelele sana za watoto, kwa hiyo ameona bora alale huku kwenye utulivu" Mlezi wa kituo cha watoto yatima alijibu wakati Jimmy na Gabby wakitoka stoo, Mlezi wa kituo cha yatima akarudishia mlango na kuelekea ukumbini ambapo Tammy Semmy alikuwa akiongea na waandishi wa habari.



    Jimmy na Gabby wakasubiri bosi wao amalize kuhojiwa na wanahabari.



    "Tayari mmemaliza?" Tammy Semmy aliwauliza wakina Jimmy mara baada ya kumaliza mahojiano,



    "Tayari mkuu" Gabby alijibu,



    "Tunaenda Wapi sasa?" Tammy Semmy aliuliza,



    "Nadhani mtaa unaofuata kuna kituo kingine" Jimmy alijibu,



    "Twendeni uko" Tammy Semmy aliongea huku akianza kupiga hatua.



    Baada ya nusu saa shughuli nzima ya kutoa misaada ilikuwa imeisha na Tammy Semmy na watu wake waliondoka eneo hilo, walielekea kwenye vituo vingine kuendelea kutoa misaada.



    Mlezi wa kituo cha kulelea watoto yatima alirudi stoo na kumuamsha Tom,



    "Kijana amka sasa uende, si uliomba kulala tu?" Mlezi wa kituo cha yatima aliongea baada ya Tom kufungua macho,



    "Mama miguu bado unaniuma na isitoshe nilikueleza toka jana kuwa sina ndugu hapa, naomba hifadhi ya siku mbili tatu ili nirudi vizuri kiafya" Tom aliongea kwa huruma,



    "Nikikupa nauli unaweza kurudi kwenu?" Mlezi wa yatima aliuliza,



    "Mama uko nitokapo ndio nimetumwa nije mjini kutafuta ajira ambayo itaniwezesha kupata pesa kidogo kwa ajili ya kuwatumia nyumbani, uko ni shida na umasikini umetawala, inaweza kupita siku mbili bila kula na ukizingatia nina wadogo zangu wadogo sana na mzazi wangu ananitegemea mimi" Tom alidanganya huku machozi yakimtoka,



    "Sasa hapa mjini utafanya kazi gani?" Mlezi wa yatima aliuliza,



    "Yoyote mimi nafanya, nipe kazi yoyote ila sio ya kutembea tembea mitaani" Tom aliongea kwa huruma,



    "Unachagua kazi sasa, kwanini hutaki za kutembea tembea mitaani?" Mlezi wa kituo aliuliza,



    "Mama mimi nina matatizo ya miguu, uwa inavimba kila nikitembea" Tom aliongea huku akijitazama miguu yake,



    "Kubeba mizigo unaweza?" Mlezi wa kituo aliuliza,



    "Nitaweza tu, kwa maana nina shida na pesa" Tom alijibu kwa upole,



    "Kuanzia leo kazi yako itakuwa ya kutoa na kuingiza vitu stoo" Mlezi wa yatima aliongea na kufanya Tom afurahi, aliamini endapo atakuwa anashinda stoo tu, ni ngumu kuonekana kwa watu wanaomtafuta.



    "Nashukuru sana mama, ubarikiwe" Tom aliongea huku akipiga magoti,



    "Kwanza amka ukanywe chai, alafu tutaongea vizuri" Mlezi wa yatima aliongea na Tom akanyanyuka kisha akaelekezwa sehemu ya kupatia kifungua kinywa huku akifurahi kupata nafasi hiyo na alipanga akusanye hela taratibu ili spate pesa ya kutosha kwa ajili ya nauli ya kutoka nje ya nchi.



    *******************



    Asubuhi ilimkuta Koplo Mbegu akiwa barabarani akitembea kwa miguu, begi lake la nguo likiwa mgongoni, alikuwa anatafuta lodge nyingine ya kuishi, aliamini pale alipokuwepo hapakuwa salama kabisa, fikra zake zilimwambia huenda Tom na kina Gabby ni watu wamoja kwa hiyo kitendo cha Tom kupajua anapoishi Koplo Mbegu, basi hata wakina Gabby watapata taharifa.



    Koplo Mbegu aliendelea kuyega bila muelekeo, ila wazo mwisho lililomjia ni kwamba aende kule nje ya mji ambapo ndipo Rais alifia, aliamini akienda kule na kisha akamtafuta yule kijana mwenye Maneno mengi basi hatokosa sehemu ya kuishi kwa muda.



    Alitafuta usafiri uliomfikisha mpaka eneo analotaka kwenda, na kwa bahati nzuri alifanikiwa kumpata yule kijana muongeaji sana,



    "Umekua hadimu kaka, hata nikikupigia simu inaita tu bila kupokelewa" Kijana mwenye Maneno mengi aliongea kwa furaha,



    "Mimi nipo, sema ile simu niliipoteza" Koplo Mbegu alijitetea,



    "Karibu kaka, umekuja na jipya gani?" Kijana mwenye Maneno mengi aliuliza,



    "Kwanza naomba unisaidie jambo moja" Koplo Mbegu aliongea na kumtupia jicho yule kijana,



    "Jambo gani kaka, sema tu usisite" Kijana mwenye maneno mengi aliongea kwa uchangamfu,



    "Nahitaji sehemu ya kuishi kwa muda" Koplo Mbegu aliongea,



    "Wapi sasa, hapa kijijini au sehemu gani?" Kijana mwenye maneno mengi aliuliza,



    "Nahitaji hapa hapa kijijini" Koplo Mbegu alijibu,



    "Sasa mbona nyumba ya hadhi yako ni ngumu sana kuipata, nyie mmeshazoea kukaa nyumba nzuri za tofali za simenti, sasa hapa kijijini nyumba zote ni tofali za tope" Kijana mwenye maneno mengi aliongea huku akitabasamu,



    "Huku nakuja kikazi, kwa hiyo sitaki kuchagua pa kukaa, nitaishi popote" Koplo Mbegu aliongea,



    "Basi twende tukaishi kwangu, nina kakibanda changu kana vyumba viwili, nitakupa chumba kimoja" Kijana mwenye maneno mengi aliongea,



    "Nashukuru sana, twende sasa" Koplo Mbegu aliongea,



    "Sasa si ukachukue kwanza nguo na vitu vingine, maana hata kitanda hakuna" Kijana mwenye maneno mengi aliongea,



    "Hapa nilipo ndio nimekuja Kamili, hayo masuala ya vitanda tutajua siku zijazo" Koplo Mbegu aliongea na kumfanya kijana mwenye maneno mengi ashangae,



    "Kaka unanishangaza, yaani hapo ndio umekuja hivyo? yaani upo Kamili?" Kijana mwenye maneno mengi aliuliza tena huku akishangaa,



    "Kwani vipi dogo?, nipo Kamili, wewe nipeleke uko kwako" Koplo Mbegu aliongea huku akijibandika tabasamu usoni mwake,



    "Eeeeh!!!! haya twende basi" Kijana mwenye maneno mengi aliongea na kisha akaanza kupiga hatua huku akifuatwa na Koplo Mbegu, safari yao iliishia kwenye nyumba mmoja ya udongo iliyokuwa na vyumba viwili na choo kilichokuwa kwa mbali kidogo na nyumba.



    Kijana mwenye maneno mengi akatoa funguo ndogo na kufungua kufuri ya chumba kimoja na kuingia ndani,



    "Hiki ndio chumba chako" Kijana mwenye maneno mengi alimwambia Koplo Mbegu huku wakiwa katika chumba ambacho hakikuwa na kitu chochote zaidi ya mkeka ulio mkuu kuu ulitandikwa upande mmoja wa chumba,



    "Shukrani, ngoja nipasafishe" Koplo Mbegu aliongea huku akiokota mfagio wa makuti uliokuwa ukizagaa chumbani hapo,



    "Ngoja nikusafishie, wewe ni mgeni bwana" Kijana mwenye maneno mengi aliongea huku akitaka kuuchukua ufagio mikononi mwa Koplo Mbegu,



    "Acha tu, nitasafisha mwenyewe, usijali dogo" Koplo Mbegu aliongea huku akizuia ufagio usichukuliwe na kijana mwenye maneno mengi,



    "Sawa basi, wakati wewe ukiendelea na usafi, ngoja mimi nifanye mpango wa chakula" Kijana muongeaji aliongea huku akielekea nje,



    "Unapika chakula gani?" Koplo Mbegu alimuuliza,



    "Wali na dagaa" Kijana mwenye maneno mengi alijibu,



    "Chukua hii, katafute kuku, leo tule kuku bwana" Koplo Mbegu aliongea huku akimpatia noti mbili za elfu kumi,



    "Mbona nyingi hivi?, huku kwetu kuku ni shilingi elfu tano tu" Kijana mwenye maneno mengi aliongea huku akitabasamu,



    "Basi itakayobaki utaninunulia maji makubwa na wewe utanunua soda yako au bia na nyingine utajua cha kufanyia" Koplo Mbegu aliongea na yule kijana akaondoka huku akitabasamu.



    Kuanzia siku hiyo Koplo Mbegu alianzisha maisha yake upya ndani ya kijiji hicho na kwa wakati huo Tom nae alianza maisha mapya ndani ya kituo cha kulelea watoto yatima.



    *********************



    BAADA YA MWEZI MMMOJA.



    Uchaguzi ulikuwa tayari umeshafanyika na siku hii ya leo ndio matokeo ya jumla yalikuwa yametangazwa na Tammy Semmy akashinda kwa asilimia kubwa sana, kwa hiyo kilichokuwa kinasubiriwa ni kuapishwa kwake katika siku inayofuata, mtandao wake wote ukawa na furaha, kila mtu aliyekuwa kwenye ule mtandao wa Tammy Semmy alianza kuwaza namna atakavyoogelea katika utajiri baada ya kuangaika kwa muda mrefu ili Tammy Semmy awe Rais.



    Na leo kulikuwa hafla ndogo kwenye kambi yao, Tammy Semmy alikuwa mwenye furaha sana,



    "Wiki ijayo ndio utaenda marekani kufanyiwa ubadilishwaji wa sura, au pia ningependekeza kuwa ubaki na sura yako alafu nitatangaza kuwaachia wafungwa kwa msamaha na wewe uwepo kati ya hao wafungwa na utaishi uraiani vizuri na sura yako hiyo hiyo ila hautakuwa na kazi serikalini" Tammy Semmy alimwambia Waziri wa ulinzi,



    "Nadhani hiyo ya kubaki na sura yako ni nzuri zaidi, alafu unakuwa huna kazi ila pesa unakuwa nazo za kutosha" Jimmy alichangia huku akimuangalia Waziri wa ulinzi,



    "Yote sawa, ila ngoja nipate muda wa kufikiria" Waziri wa ulinzi alijibu,



    "Gabby na Jimmy nawashukuru sana, ahadi niliyowapa ni kuwa kila mmoja nitamnunulia nyumba marekani na pia nitawapa mgodi mmoja muwe mnaumiliki" Tammy Semmy aliongea na kisha Gabby na Jimmy wakagongana mikono kwa furaha,



    "Asante sana mkuu" Gabby aliongea huku akicheka kwa furaha,



    "BQ nilikutoa kwenye kikundi cha ujasusi chini ya nchi ya urusi, na nilikuhaidi kukupa mgodi mkubwa mmoja na pia nilikuahidi kukupa sehemu kubwa ya ardhi katika mji wetu mkubwa wa kibiashara ili ujenge majengo yako ya biashara kwa pesa ya serikali yetu, lakini kwa jinsi mambo yalivyo, ni lazima uchague moja kati ya hayo mawili, alafu litakalobaki tutaingia ubia kati yangu na yako, yaani tutachangia hisa" Tammy Semmy aliongea huku akimuangalia BQ,



    "Hapo inakuwa unatoka nje ya makubaliano" BQ aliongea huku akiwa hana furaha tena,



    "Sio hivyo, nimeangalia nimeona ni vyema tuchangie kimoja kwa maana ukitoa masuala ya migodi na majengo ya kibiashara, hakuna kitu kingine cha kuingiza pesa nyingi" Tammy Semmy alijitetea,



    "Fuata maelekezo ya mkataba tulioingia mimi na wewe, achana na maelezo mengine" BQ aliongea kwa ukali,



    "Mkataba ni makaratasi tu, yanaweza kuchanwa au kuchomwa moto" Tammy Semmy aliongea kijeuri,



    "Sawa haina shida" BQ aliongea na kunyanyuka, akaondoka zake kwa hasira na kuwaacha wenzake wakitazamana,



    "Ila kweli, haiwezekani achukue mali nyingi hivyo" Waziri wa ulinzi aliongea,



    "BQ anatakiwa auawe haraka iwezekanavyo" Tammy Semmy aliongea huku akiwatazama Gabby na Jimmy.........





    "Kwanini tusiongee nae tu kwa kumbembeleza ili akubali kupokea unachompa?" Waziri wa ulinzi aliuliza,



    "Hivi unawajua majasusi wewe? yaani ukishafanya nae makubaliano basi timiza kama mlivyokubaliana, vinginevyo ni kifo tu, yaani atamuua yule aliyevunja makubaliano" Tammy Semmy aliongea,



    "Kwa hiyo unataka kuniambia ni lazima akuue?" Waziri wa ulinzi alimuuliza Tammy Semmy,



    "Mkuu kuua hawezi, kwanza sasa hivi ulinzi wako utakuwa maradufu" Jimmy aliongea,



    "Nyie hamumjui vizuri huyu binti, muangalieni hivyo hivyo na kumuacha" Tammy Semmy aliongea huku akitabasamu,



    "Kwa hiyo tufanyaje sasa?" Gabby aliuliza,



    "Anatakiwa auawe" Tammy Semmy alijibu,



    "Tumfuate kwake basi tukammalize muda huu" Gabby aliongea,http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    "Kwa mtindo huo wa kumvamia, hakuna atayerudi mzima kati yenu, yule anatakiwa auawe huku mkiwa pamoja mkiongea nae na kufurahi kama marafiki" Tammy Semmy aliongea,



    "Kwa hiyo tunafanyaje sasa?" Waziri wa ulinzi akauliza,



    "Ngojeni kesho nitamuita hapa na tutaweka mambo vizuri ili aniamini kama zamani, alafu kesho kutwa wote tutasafiri kwa ajili ya kwenda kujipongeza mbuga ya wanyama, uko ndipo atakapofia" Tammy Semmy alizungumza,



    "Alafu akishakubali kwenda uko mbugani tutafanyaje?" Waziri wa ulinzi aliuliza,



    "Sasa tukifika nae tunamuwasha shaba tu, alafu tunamuacha uko aliwe na wanyama" Tammy Semmy aliongea,



    "Wazo zuri sana" Waziri wa ulinzi alimpongeza Tammy Semmy,



    "Sasa jiandaeni kwa safari, kesho kutwa mapema tunaondoka wote" Tammy Semmy aliongea,



    "Kwa hiyo leo tupo free?" Jimmy aliuliza,



    "Free kivipi?, kamtafuteni Tom na huyo askari angalieni anafanya kazi kituo gani ili muweze kumpata kirahisi na mummalize haraka" Tammy Semmy aliongea huku huku akiinuka,



    "Ni wazo zuri" Gabby aliongea huku akivaa shati lake,



    "Sasa mimi naenda nyumbani kupumzika, si mnajua kesho ndio siku yangu ya kuapishwa?" Tammy Semmy aliongea huku akifuta kiatu chake,



    "Kapumzike tu mkuu" Jimmy alijibu huku akijichekesha.



    Tammy Semmy akaondoka zake na baada ya nusu saa Gabby na Jimmy walipanda gari na kuondoka, safari yao walipanga kuishia kwenye kituo kikuu cha polisi kwa ajili ya kufuatilia mwenendo wa Koplo Mbegu.



    Walifika kituoni na kuomba kuonana na mkuu wa polisi, wakaelekezwa ofisi ilipo na kwenda moja kwa moja, walipofika walimkuta mkuu wa polisi na kukaribishwa.



    Mkuu wa polisi alishamtambua Gabby kutokana na picha waliyoiona yeye na Koplo Mbegu,



    "Karibuni vijana" Mkuu wa polisi aliongea huku akisoma makabrasha yake yaliyokuwa mezani,



    "Asante mkuu, tuna shida ndogo kidogo" Gabby aliongea,



    "Shida gani?" Mkuu wa polisi aliuliza huku akivua miwani yake ya macho,



    "Tunamuulizia askari mmoja anaitwa Said Mbegu" Gabby aliongea,



    "Ila hamjajitambulisha kwanza" Mkuu wa polisi aliongea huku akitabasamu,



    "Sisi ni maofisa wa usalama wa taifa" Jimmy alitoa jibu,



    "Sawa, kwanini mnamtamfuta huyo askari?" Mkuu wa polisi aliuliza,



    "Kuna tukio limetokea ambalo ni nyeti, na yeye kwa kiasi fulani ameonekana kuhusika, hatujaja hapa kumchukua ili tukamuhadhibu, lah, tumekuja kumchukua ili tukamuhoji" Gabby aliongea,



    "Sawa kabisa, ila huyo mtu mnaemtaka ni kwamba hajaripoti kazini karibia miezi miwili na simu zake hazipatikani na mbaya zaidi hata kwake ametoweka, na majirani hawajui alipo" Mkuu wa polisi aliongea,



    "Kwao kabisa ni wapi? yaani kwa wazazi wake" Jimmy aliuliza,



    "Kwakweli sijui, si unajua hatuwezi kufuatilia chimbuko la kila mfanyakazi wa hapa?" Mkuu wa polisi aliongea,



    "Na marafiki zake wa karibu au mpenzi wake unawajua?" Jimmy aliuliza,



    "Hapana" Mkuu wa polisi alijibu,



    "Sawa tunashukuru, tutarudi tena ikibidi" Gabby aliongea huku akinyanyuka na Jimmy nae akainuka,



    "Sawa, karibuni tena" Mkuu wa polisi akaongea,



    "Tumeshakaribia, hapa ni nyumbani" Jimmy akaongea huku akitabasamu kisha wakaondoka na kumuacha mkuu wa polisi akiwaangalia kwa jicho makini.



    Baada ya Gabby na Jimmy kutoka, mkuu wa polisi aliichukua simu yake na kumpigia Koplo Mbegu kumpa taharifa ya kutafutwa na watu hao.



    ******************



    Koplo Mbegu baada ya kukata simu aliyopigiwa na mkuu wake, aliichukua gazeti lake na kusimama. Muda huo alikuwa mjini kwenye mgahawa, baada ya kusimama alilipia huduma aliyopewa na kuanza kuelekea nje ya mgahawa na alichokifanya muda huo ni kwenda katika chumba chake cha pale mjini.



    Alifika na kukuta kama kilivyokuwa hawali ingawa kuna sehemu zilikuwa zimepekuliwa pekuliwa, macho yake yakagota kwenye simu yake mezani, akaichukua na kuiona imezima, akahisi ni chaji imeisha, akaichomeka kwenye chaji na kisha akaiwasha, kitu cha kwanza akaenda kwenye missed call na kukuta namba nyingi za rafiki zake zikiwa zimempigia, ila hakujali, macho yake yaligota kwenye namba mpya iliyokuwepo kwenye kioo cha simu yake, kitu ambacho hakujua ni kuwa hiyo namba ni namba ya BQ.



    Koplo akataka kupiga ila roho yake ikasita, akaichukua ile namba na kuifadhi kwenye simu yake anayoitumia muda huu na kisha ile simu yake ya zamani akaizima na kisha akachukua mashuka yake mawili mazito na kuyatia kwenye begi na kuondoka zake.



    Akaenda akatafuta usafiri wa kumfikisha katika kijiji anachoishi kwa sasa, baada ya kupata usafiri alienda mpaka kujijini na aliposhuka kwenda usafiri huo akaelekea moja kwa moja mpaka kwenye makazi yake mapya na kumkuta kijana mwenye maneno mengi akiwa anatayarisha samaki kwa ajili ya maandalizi ya mlo wa mchana,



    "Hivi huna hata hawara awage anatupikia?" Koplo Mbegu alimtania kijana mwenye maneno mengi,



    "Aaah kaka, wanawake wanataka mtu mwenye hela kaka" Kijana mwenye maneno mengi alijibu huku akicheka,



    "Basi Fanya kitu kimoja, tafuta msichana awage anatupikia chakula, alafu wewe uwe unafanya shughuli zako muda huu, mimi sipendi kuona wewe unapika alafu unaacha shughuli zako" Koplo Mbegu aliongea huku akikaa kwenye kigoda,



    "Sina shughuli yoyote kaka, mimi maisha yangu nategemea kilimo, sasa mvua zimegoma msimu huu kwa hiyo naishi kwa kuunga unga tu" Kijana mwenye maneno mengi aliongea,



    "Basi tafuta binti awe anatupikia hapa, alafu wewe niambie unataka biashara gani?" Koplo Mbegu alimuuliza,



    "Mabinti wapo wengi tu, kesho nitamleta hapa" Kijana mwenye maneno mengi aliongea,



    "Alafu biashara gani utapenda ufanye?" Koplo Mbegu alimuuliza,



    "Napenda sana kuuza mitumba, ningekuwa na pesa ningekuwa nafuata nguo mjini na kuja kuuza huku" Kijana mwenye maneno mengi aliongea huku akicheka,



    "Basi nitakupa hela jioni ili kesho ufuate mitumba mjini" Koplo Mbegu aliongea na kufanya kijana mwenye maneno mengi afurahi,.



    "Yaani ujio wako ni kama ujio wa malaika mwema, maana tokea umekuja hata msosi napiga mara tatu kwa siku, tena msosi wa nguvu tu, mpaka ukija kuondoka nitakuwa nimenenepa" Kijana mwenye maneno mengi aliongea kwa bashasha,



    "Usijali, hao samaki unawapika na chakula gani?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Ugali tu, yaani hawa samaki nawakaanga na kisha napika na mboga za majani na ugali" Kijana mwenye maneno mengi aliongea,



    "Basi sawa, acha mimi nijipumzishe kidogo ndani" Koplo Mbegu aliongea huku akinyanyuka kwenye kigoda,



    "Wewe lala tu kaka, acha mimi nirekebishe mambo" Kijana mwenye maneno mengi aliongea wakati Koplo Mbegu akiingia chumbani kwake.



    **********************



    Tom yeye alikuwa ndani ya nyumba ya kulea yatima na muda huu wa mchana ndio alikuwa ametoka kumaliza kusafisha nyumba hiyo na sasa alikuwa stoo anataka ajipumzishe kidogo kwa nusu saa huku akisubiri muda wa chakula cha mchana.



    Hata kabla hajaanza kusinzia, alikuja mlezi wa kituo cha kulea yatima na kusimama mbele yake,



    "Hivi ulisema huna ndugu hapa?" Mlezi wa kituo alimuuliza,



    "Ndio mama" Tom alijibu,



    "Kuna mtu anakuulizia hapo nje, anadai unamfahamu" Mlezi wa kituo aliongea na moyo wa Tom ukapata mshtuko,



    "Huyo mtu yupoje? mwanamke au mwanaume?" Tom aliuliza maswali mfululizo,



    "Nenda kamuone" Mlezi wa kituo alijibu huku akitoka,



    "Mwambie aje" Tom aliongea huku wasiwasi ukizidi kumjaa, aliamini ni Koplo Mbegu amekuja,



    "Huyu hapa anakuja" Mlezi wa watoto aliongea huku akiondoka na kumfanya Tom akae pale stoo huku akisubiri kumuona huyo mtu.



    Baada ya sekunde chache huyo mtu alisimama mlangoni na kumuangalia Tom. Tom akatamani hata apae ili akimbie lakini haikuwezekana.........







    Japo Tom alitamani ardhi ipasuke ila haikuwezekana, yule mtu aliendelea kusimama mlangoni huku akimuangalia Tom alivyofadhaika,



    "Mtu asiye na nguo" Tom aliongea peke yake huku yule mtu akiwa jirani kabisa,



    "Kwanini unaniogopa?" Sudy Bakari alimuuliza Tom,



    "Mbona sikuogopi" Tom aliongea huku macho yake yakionesha uoga aliokuwa nao, Sudy bakari akatabasamu,



    "Nahitaji kuongea na wewe" Sudy Bakari aliongea,



    "Sawa, twende eneo la wazi, kuogelea stoo sio vizuri" Tom alijibu ila aliamua wakaongelee nje kwa sababu ya kuogopa kudhuliwa ndani ya stoo na akakosa msaada.



    Wakatoka mpaka eneo la nje lakini ndani ya geti la kituo cha kulea yatima, wakatafuta sehemu yenye viti na kukaa.



    "Kiumbe umejaa matatizo, ila hujui namna ya kujisaidia, mimi naujua mwanzo wa matatizo yako, nilikuwepo siku ile wakati rais anauawa na najua wewe hujaua" Sudy Bakari aliongea na kufanya Tom amtolee macho kwa maana aliona huyu mtu ndio mwenye kujua ukweli, ila Tom alipata hofu baada ya kuona macho ya Sudy Bakari sio ya kawaida, yalikuwa ya kibuluu na mboni yake ilikuwa ndogo sana kama nukta ya penseli,



    "Sasa hata kama unaujua ukweli, huwezi kunisaidia, hawa watu wanamtandao mpana" Tom aliongea kwa hofu,



    "Kweli siwezi, ila nipo upande wa haki" Sudy Bakari aliongea,



    "Kama huwezi basi sioni haja ya kuongea kuhusu habari hizo" Tom aliongea,



    "Kiumbe dhaifu mbona unakata tamaa mapema? Enyi wenye asili ya udongo mna mawazo magumu ila mioyo laini, kwanini msiwe kama sisi?" Sudy Bakari aliuliza,



    "Unaposema sisi wenye asili ya udongo unamaanisha nini?" Tom akamuuliza,



    "Wanadamu mmeumbwa kwa udongo, si ndio?" Sudy Bakari aliuliza,



    "Ndio, na unaposema tungekuwa kama nyinyi pia unamaanisha nini? wewe sio mwanadamu?" Tom alimuuliza tena,



    "Sijaja kujibu maswali ya namna hiyo, ninachotaka ni kusimamia haki ya dunia yako" Sudy Bakari alijibu,



    "Kama huwezi kunisaidia ni vipi utaweza kusimamia haki yangu?" Tom aliuliza,



    "Anayeamini pasipo kuona ndio mwenye imani kubwa, ila anaeona na haamini huyo hafai kuwa muamini" Sudy Bakari alijibu huku akisimama,



    "Mafumbo yako hayanisaidii kitu, na kwanini una uwezo wa kupotea na kuingia ndani mlango ukiwa umefungwa?" Tom aliuliza tena,



    "Na wewe ni kwanini hauwezi kuingia ndani mpaka mlango uwe wazi?" Sudy Bakari aliongea huku akiwa amesimama,.

    .



    "Binadamu ndivyo tulivyo" Tom alijibu,



    "Basi tofauti yetu ipo hapo" Sudy Bakari alijibu huku akiwa amesimama,



    "Ipo wapi?" Tom aliuliza,



    "Kwenye ubinadamu" Sudy Bakari alijibu kisha akaanza kuondoka na kumuacha Tom akimuangalia,



    "Labda jini" Tom aliwaza wakati Sudy Bakari akimalizikia kutoka nje ya geti.



    Tom akaamua aende kuchukua chakula tu, muda ulikuwa umeshafika.



    ******************



    Koplo Mbegu alichelewa kuamka siku ya leo, alikuta mwenzake ameandaa chai tayari,



    "Leo umelala sana bro" Kijana mwenye maneno mengi alimwambia Koplo Mbegu,



    "Aisee we acha tu, vipi lakini?" Koplo Mbegu alimuuliza,



    "Nilikuwa nakusubiri uamke ili unipe hela kama tulivyoongea jana" Kijana mwenye maneno mengi aliongea,



    "Aaah ile biashara ya mitumba, ulisema mtaji ni shilingi ngapi vile?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Elfu ishirini tu" Kijana mwenye maneno mengi aliongea kisha Koplo Mbegu akarudi chumbani kwake, baada ya muda alitoka nje huku akiwa na pesa mkononi,



    "Chukua hii elfu hamsini, alafu angalia nguo kuendana na mazingira ya huku, usichukue nguo za bei ghali, hautouza" Koplo Mbegu aliongea huku akimkabidhi zile pesa,



    "Elfu hamsini bro? Nyingi sana hii" Kijana mwenye maneno mengi aliongea huku akirudisha baadhi ya pesa,



    "Kaa nayo yote, alafu vipi kuhusu msosi wa mchana kama ukiondoka?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Chungulia jikoni" Kijana maneno mengi aliongea huku akicheka na kumfanya Koplo Mbegu atupe jicho jikoni na kumuona binti akichagua mchele,



    "Ndio mpishi wetu leo" Kijana mwenye maneno mengi aliongea huku akicheka,



    "Sawa, basi mimi naenda kujimwagia maji, leo nitashinda hapa, sitotoka" Koplo Mbegu aliongea huku akielekea bafuni,



    "Poa kaka, baadae basi" Kijana mwenye maneno mengi aliongea huku akiondoka zake,



    "Poa" koplo Mbegu alijibu kisha akapotelea bafuni.



    Baada ya nusu saa Koplo Mbegu alikuwa ameshakunywa chai tayari na alikuwa amejipumzisha chini ya mti, ndipo akakumbuka kuna namba mpya aliikuta imempigia kwenye ile simu yake ya zamani, Koplo Mbegu akaamua aipige ile namba, namba iliita tu muda mrefu bila kupokelewa, akajaribu tena, hali ikawa ile ile, akaamua ahache kuipiga, kisha akaanza kuangalia habari zilizojiri leo kupitia mitandao ya kijamii.



    ****************



    Muda huu wa asubuhi hii ndani ya kambi ya Tammy Semmy kulikuwa na kikao kidogo cha mapatano baina ya Tammy Semmy na BQ,



    "Nimeona sio vyema kuvunja makubaliano, mkataba wangu na wewe utakuwa vile vile kama hawali" Tammy Semmy aliongea kinyenyekevu,



    "Sawa, ila mimi nilishapanga kuondoka kesho" BQ alijibu,



    "Hapana usiondoke, maana usiku wa leo nimepanga tusafiri kwa mapumziko ya wote twende mbuga za wanyama angalau tukakae siku mbili, alafu baada ya hapo kila mtu ataenda kupumzika katika nchi anayoitaka" Tammy Semmy aliongea,



    "Tayari nina tiketi lakini" BQ aliongea,



    "Tutanunua nyingine, hiyo uliyonayo irudishe au toa sadaka" Tammy Semmy aliongea kwa kujiamini,



    "Basi nashukuru kwa kukubali kuzingatia mkataba wetu, muda huu naomba nikajiandae kwa hiyo safari ya jioni ya kwenda mbuga za wanyama" BQ aliongea,



    "Hutakiwi kuondoka, sasa hivi wote mnapaswa kuongozana na mimi ili tuelekee uwanja wa Taifa nikaapishwe" Tammy Semmy aliongea,



    "Sawa haina shida" BQ aliongea huku akielekea kwenye friji ambapo alitoa chupa ya soda na kuifungua kwa mkono na kuanza kunywa,



    "Nyie wanaume kavaeni suti, BQ nadhani ulivyovaa hivyo hivyo ni sahihi" Tammy Semmy aliongea kisha jimmy na Gabby wakaelekea vyumbani mwao kuvaa suti na kipindi hiki simu ya BQ ilikuwa inaita na ni namba ngeni ilitokea kwenye simu yake, akaipuuza kwa muda huo ila alifanya kosa kuipuuza, kitu ambacho hakujua ni kuwa hiyo namba ni ya Koplo Mbegu.



    Baada ya muda vijana walikuwa wameshajiandaa na Tammy Semmy akatoka nao, safari ya kwenda uwanjani kuapishwa ilikuwa imeanza rasmi, ndani ya gari kila mtu alikuwa kimya akiwaza jambo lake, ila Tammy Semmy alichokuwa akiwaza kwa muda huo ni juu ya kifo cha BQ.



    *********************



    ________________________

    SIKU YA KIFO CHA BQ..

    ________________________



    Siku mpya iliwakuta Tammy Semmy na wenzake wakiwa ndani ya hotel moja ya kifahari iliyojengwa ndani ya mbuga ya wanyama, na sasa Tammy Semmy alikuwa Rais kamili kutokana na kuapishwa katika siku iliyopita.



    Tammy Semmy na watu wake walikuwa wamekaa kwenye meza wakisubiri muda ufike waanze kuzungushwa mbugani,



    "Mheshimiwa, twendeni" Mfanyakazi wa mbuga za wanyama alikuja na kuongea kisha Tammy Semmy na wenzake wakanyanyuka na kuanza kumfuata, walitembea mpaka eneo moja ambalo lilionekana ni uwanja wa ndege na ndege ndogo mbili zilikuwa mbele yao,



    "Tumeona tuanzie kuzunguka na ndege, alafu jioni tutatumia gari" Mfanyakazi wa mbugani aliongea huku akimtazama Tammy Semmy,



    "Haina shida, ila hizi ndege mbona ndogo? tutaenea kweli?" Tammy Semmy aliuliza,



    "Zinatosha watu wanne, yaani pamoja na rubani, itabidi niondoke na watu watatu, alafu nitawashusha na kuchukua wengine wawili waliobaki" Rubani wa ndege aliongea,



    "BQ we si unaweza kuendesha ndege?" Tammy Semmy alimuuliza BQ,



    "Naweza" BQ alijibu huku akitabasamu,



    "Sasa itabidi moja uendeshe moja" Tammy Semmy aliongea,



    "Haina shida, nitapanda na nani?" BQ aliuliza,



    "Utapanda na mimi" Tammy Semmy aliongea huku akitabasamu,



    "Sawa, twende" BQ aliongea huku akimuangalia,



    "Ila kwanza ruka nayo mwenyewe ili nihakikishe kama upo vizuri" Tammy Semmy aliongea huku akitabasamu,



    "Haina shida, ila itabidi tuwe wawili ndani ya ndege ili iwe nzito kidogo" BQ aliongea na kufanya wenzake watazamane kwa muda,



    "Nenda Waziri" Tammy Semmy aliongea huku akimuangalia Waziri wa ulinzi, lakini Waziri wa ulinzi alionekana kusita,



    "Kwanini asiende peke yake?" Waziri wa ulinzi aliongea huku akionekana kugoma kuambatana na BQ,



    "Nenda tu, hatutafanya chochote kibaya" Tammy Semmy aliongea kwa sauti ndogo huku akiwa jirani na Waziri wa ulinzi na kufanya BQ azidi kupata mashaka,



    "Nawaamini" Waziri wa ulinzi aliongea kwa sauti huku akielekea kupanda ndege, BQ nae akaenda akapanda ndege na kuwaacha chini rubani, Tammy Semmy na vijana wake.



    "Sasa tunafanyaje mkuu, mbona Waziri wa ulinzi nae amepanda?" Rubani aliuliza, inaonekana kabisa huyu rubani nae yupo kwenye mtandao wa Tammy Semmy,



    "Kwani rimoti ya kulipulia bomu ipo wapi?" Tammy Semmy aliuliza,



    "Hii hapa" Rubani aliongea huku akiitoa rimoti mfukoni na wakati huo ndege aliyokuwa anaendesha BQ ilikuwa inachukua kasi ili iruke,



    "Itabidi tuilipue tu, tukimkosa BQ hapa, basi hatutoweza tena kumuua" Tammy Semmy aliongea,



    "Sasa Waziri wa ulinzi si yupo, kwa hiyo nae afe?" Jimmy aliuliza kwa mshangao,



    "Hakuna namna, itabidi afe tu ili tuokoke wengi" Tammy Semmy aliongea na kufanya wenzake wakae kimya.



    Ndani ya ndege muda wote BQ alikuwa akitabasamu ila waziri wa ulinzi alionekana mwenye wasiwasi sana.



    BQ alianza kuirusha ndege na ndege ikaenda hewani na kumfanya atabasamu,



    "Mbona huna raha mkuu?" BQ alimuuliza Waziri wa ulinzi wakati ndege ipo juu,



    "Hakuna kitu, nilikuwa na uoga na uwezo wako wa kurusha ndege" Waziri wa ulinzi aliongea,



    "Mh....nasikia sauti kama ya alarm kwa mbali" BQ aliongea baada ya kusikia sauti ya alarm inayopiga kwa kasi ya sekunde ya saa,



    "Hata mimi nasikia, inatokea siti za nyuma" Waziri wa ulinzi aliongea, ila yeye alishajua kuwa hilo ni bomu lililotegwa ndani ya ndege hiyo,



    "Itakuwa ya mafuta au injini?, ila mbona nikiviangalia vyote navyoona vipo sawa?" BQ aliuliza huku akivua headphones za mawasiliano na kutaka kwenda upande wa nyuma ambayo sauti ya alarm ilikuwa ikitokea, akasogea na kuona kitu kikiwa na taa nyekundu ikiwaka na kuzima,



    "Bomu" BQ alijikuta akiongea peke yake na na akatajaribu kutaka kujiokoa, alirudi mpaka kwenye mlango wa ndege huku akipiga hesabu za kuruka chini akiwa pale mlangoni, na wakati huo ndipo Tammy Semmy nae alikuwa anabonyeza kitufe cha kulipulia bomu, ndege ikalipuka na kutawanyika vibaya sana hata kabla BQ hajaruka na ikaangukia kwenye maporomoko ya maji huku ikiwaka moto.



    Tammy Semmy na wenzake walilishuhudia tukio lile ila kati yao hakuna aliyeonekana kuwa na furaha kutokana na mwenzao ambaye ni Waziri wa ulinzi kuwepo ndani ya ndege hiyo..........







    Tammy na wenzake wakachukua gari na kuanza kuelekea sehemu ambapo ndege ililipukia na muda huo tayari wafanyakazi wengine wa mbuga za wanyama walishatoka nje baada ya kusikia mlipuko huo.



    Gari ile ilisogea mpaka ndege ilipolipukia na kukuta ile ndege imeangukia kwenye maporomoko ya maji ila waliweza kukuta vipande kadhaa vya ndege ile vikiendelea kuungua, wakaanza kukagua ili waone kama wataweza kumuona mtu yoyote aliyekuwepo ndani ya ndege ile lakini hawakubahatika kuona kitu,



    "Twendeni upande wa kule chini maporomoko yanapoangukia" Rubani wa ndege aliongea na kisha wakaanza kuelekea uko.



    Walitembea kwa mguu mpaka chini ya maporomoko hayo na chini kulikuwa na mto ambao ulisheeni mamba. Wakaanza kukagua tena kwa kuyaangalia yale maji ya mto kwa muda, waliendelea kuwepo eneo lile kwa muda kiasi kwamba wakaanza kukata tamaa ya kuiona miili ya wenzao, wakiwa wanataka kuanza kuondoka wakaona shati alilovaa Waziri likiibuka juu ya maji,



    "Watakuwa maeneo haya" Jimmy aliongea huku wakishuhudia lile shati likielea juu, wakiwa bado wapo hapo waliweza kushuhudia kiganja cha mkono wa mtu kikitupwa ufukweni kwa wimbi la maji, Gabby akachukua kijiti na kukisogeza kile kiganja nchi kavu na kuanza kukikagua,



    "Mkono wa BQ huu" Jimmy aliongea baada ya kuona pete kwenye kidole kimoja cha kile kiganja na wakati huo huo wakashuhudia fulana aliyovaa BQ nayo ikielea juu ya maji,



    "Tayari kazi imeisha, wameshakufa" Tammy Semmy aliongea,



    "Labda tungeona miili yao ndio tungehakikisha" Gabby aliongea,



    "Tayari hapo, mamba uwa awahachi kitu" Rubani aliongea,



    "Sasa twendeni, kazi imeisha" Tammy Semmy aliongea huku akianza kuondoka na wenzake wakamfuata



    Walirudi mpaka walipoegesha gari lao na kupanda kisha wakarudi hotelini kila mmoja akaenda kwenye chumba alichofikia na kila mmoja alikuwa na wazo lake kuhusu tukio lile lililotokea muda mchache uliopita, Gabby na Jimmy hawakuonekana kufurahia kabisa kitendo cha Waziri wa ulinzi kuuawa, ila kwa upande wa Tammy Semmy kwake ilo hakujali sana, alichokuwa anakijali ni BQ kufa, kwa maana aliujua uwezo wake, aliamini kabisa BQ akiendelea kuishi ni lazima maisha yake yangekuwa hatarini hata kama atazungukwa na walinzi mia kila hatua anayopiga.



    Tammy Semmy baada ya kuingia chumbani kwake, alivua viatu na kuchukua simu yake ya mkononi na kupiga simu ikulu, akiwapa taharifa juu ya tukio lililotokea, ila aliwaambia ile ndege aliyotakiwa apande yeye ililipuliwa na watu wasiojulikana, kwa hiyo akadai kuwa huenda katika mbuga hizo hakuna usalama na alichopanga ni kubadili kila kitu mbugani hapo, kuanzia uongozi mpaka watumishi.



    "Sasa nafasi hii nitawapachika watu wangu, kila kitengo muhimu ni lazima kiwe chini ya wanamtandao wangu" Tammy Semmy aliongea baada ya kukata simu, kisha akachukua simu iliyokuwa mezani kwa ajili ya Huduma za hapo hotelini, akawapigia wahudumu na kuagiza chakula.



    **********************



    Tom akiwa anaendelea na kazi zake huku akisikiliza radio kupitia simu yake ndogo, ndipo aliposikia habari ambayo waandishi wanadai ni habari iliyowafikia hivi punde, habari yenyewe ilikuwa ni ile ya kuhusu ndege ndogo iliyokuwa kwenye msafara wa Rais mpya, Tammy Semmy kulipuka ikiwa angani na watu wawili wa karibu wa Tammy Semmy inasemekana wamepoteza maisha.



    Habari hiyo ilikuwa nzuri kidogo kwa Tom kwa maana hakupenda watu hao wawepo duniani, aliamini watu hao ndio chanzo cha maisha yake kuharibika.



    Tom aliendelea kufanya usafi huku akiumiza kichwa chake kujua watu hao waliopoteza maisha ni wakina nani?



    Alipomaliza kufanya usafi alielekea moja kwa moja kwa mpishi ili amuadhime simu, kwa maana simu ya mpishi ilikuwa na uwezo wa kuingia kwenye mitandao ya kijamii kwa hiyo Tom aliamini huko anaweza kupata picha juu ya watu waliokufa kwenye msafara huo wa rais.



    Baada ya kupewa simu, Tom aliingia kwenye mitandao ya kijamii kupitia account yake, na kama dhamira yake ilivyomtuma, aliweza kuona watu hao ambao inasemekana wameuawa, aliwaona kupitia ukurasa wa habari za kituo kimoja cha Taifa, na picha hizo zilikuwa ni za BQ na Waziri wa ulinzi.



    Tom alifurahi sana kwa maana hao ni watu muhimu sana waliokuwa wanampa nguvu Tammy Semmy, sasa Tom aliamua kufanya kitu muda huo, aliichukua ile picha ambayo Waziri ulinzi alivyokuwa muda huu, yaani akiwa na ndevu nyingi, kisha akaichukua na ile ya zamani wakati Waziri wa ulinzi akiwa madarakani na kuziambatanisha zote pamoja na juu ya zile picha aliandika swali lililosomeka, HUYU NDIYE YULE WAZIRI WA ULINZI ALIYEHUKUMIWA KWENDA JELA MAISHA, SASA IMEKUWAJE ATEMBEE KUTALII NA RAIS WETU MPENDWA?



    Tom baada ya kumaliza kuandika maneno hayo, aliyapost katika mtandao wa kijamii huku akiambatanisha na hizo picha za Waziri wa ulinzi, kisha akampatia mpishi simu yake na yeye akaenda zake stoo kupumzika.



    ************



    Mchana ulimkuta Koplo Mbegu akiwa chini ya mti huku akipitia magazeti, baada ya muda akachukua simu yake na kuipigia tena ile namba ngeni ambayo hakuijua, ila safari hii ile namba haikuita kabisa, akaitupa simu pembeni na kuendelea kusoma gazeti.



    Simu yake ikaanza kuita, alipoangalia jina la mpigaji simu aliona ni mkuu wa polisi, akaipokea haraka,



    "Ndio mkuu" Koplo Mbegu aliongea baada ya kupokea,



    "Umesikia kuwa Rais ameponea chupuchupu kuuawa?" Mkuu wa polisi aliuliza,



    "Ndio, nimesikia, vipi mmegundua chochote?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Hapana, ila kuna jambo jipya limezuka baada ya watu wanaosemekana kuuawa kugundulika" Mkuu wa polisi aliongea,



    "Lipi?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Kuna kijana ameweka picha kwenye mitandao ya kijamii inayosema mmoja kati ya wale waliouawa ni Waziri wa ulinzi wa zamani ambaye inasemekana yupo gerezani" Mkuu wa polisi aliongea,



    "Ni kweli au?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Tumefuatilia tumegundua ni kweli" Mkuu wa polisi aliongea,



    "Sasa imekuwaje yupo huru na kwanini aambatane na Rais?" Koplo Mbegu aliuliza,.



    "Ilo bado hatujajua, ila tulitaka kumkamata huyo kijana, ila usalama wa Taifa wamesema wao ndio wataoenda kumkamata" Mkuu wa polisi aliongea,



    "Mmeshafahamu anapopatikana huyo kijana?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Tumefuatilia kulingana na mtandao na line aliyotumia, tumegundua yupo maeneo ya mjini kwenye kituo cha kulea yatima" Mkuu wa polisi alijibu,



    "Anatumia jina gani mtandaoni ili na mimi nikazione hizo picha?" Koplo Mbegu aliuliza,.



    "Anajiita hidden journalist, kwenye profile yake ameweka picha ya camera" Mkuu wa polisi alijibu,



    "Sawa, baadae" Koplo Mbegu alijibu na mkuu wa polisi akakata simu.



    Koplo Mbegu akachukua simu yake kubwa na kuingia kwenye mtandao wa kijamii na kulitafuta hilo jina alilopewa na mkuu wa polisi, hakupata shida kulipata na kweli akazikuta hizo picha za Waziri wa ulinzi akaziona na kukiri kabisa ni yeye.



    Lakini akaendelea kupekua ule ukurasa uliopost zile picha na mwisho akakutana na picha za huyo hidden journalist, kilichomshangaza ni kuona huyo mtu ni Tom, mtu ambaye anamtamfuta muda mrefu.



    Koplo Mbegu akachukua simu na kumpigia mkuu wa polisi huku akimfahamisha kuwa mtu huyo aliyepost hizo picha ndiye mtuhumiwa wa mauaji ya Rais na Waziri mkuu. Mkuu wa polisi akashtuka na kumtaka Koplo Mbegu aende kumfuatilia huyo mtu kabla hajachukuliwa na usalama wa Taifa.



    Haraka Koplo Mbegu akaenda na kubadilisha nguo, kisha akaekekea mjini kwenda kumuwahi Tom kwenye kituo cha kulelea yatima.



    ******************



    Gabby na Jimmy walipewa taharifa juu ya mtu aliyepost picha za Waziri mkuu, wakamfuatilia na wao na kugundua kuwa ni Tom, walichofanya ni kuchukua ndege binafsi iliyowatoa mbuga za wanyama na kuwapeleka mjini kwa ajili ya kwenda kumkamata Tom, na wao wenyewe ndio waliotoa neno kuwa Tom asikamatwe na polisi ila akamatwe na usalama wa Taifa.



    Walifika Salama na kuchukua gari ya serikali iliyowafikisha moja kwa moja kwenye kituo cha kulelea yatima.



    Muda huo Tom alikuwa yupo stoo anajiandaa kutoa kiroba cha unga kwa ajili ya kupeleka jikoni.



    Gabby na Jimmy wakaingia kibabe getini na huku sura zao zikiwa na hasira tele, walikuwa wanatembea kwa haraka kuwahi ofisini kwa mlezi wa kituo na mbele yao alikuwepo Tom huku kiroba cha unga kikiwa mgongoni.......





    Uzuri ni kwamba Tom aliwapa mgongo na jinsi alivyochafuka na unga kiasi kile, ilikuwa ngumu kumtambua, kwa hiyo wao wakaingia ofisi ya mlezi wa kituo, Mlezi wa kituo aliwatambua haraka kwa maana walikuja siku chache zilizopita kuleta misaada na walikuwa wameambatana na Tammy Semmy.



    "Tumerudi tena ila kwa kikazi zaidi, sisi ni wanausalama" Jimmy aliongea baada ya kusalimiana na mama mlezi wa kituo,



    "Nini tena, mbona leo wanausalama mmeamka na mimi?" Mlezi wa yatima aliuliza kwa kunung'unika,



    "Kuna wengine walikuja kwani?" Gabby aliuliza huku wasiwasi ukimuingia,



    "Wamekuja wanajeshi hapa, wamemchukua mpishi wangu na hawajasema sababu" Mlezi wa kituo cha yatima aliongea,



    "Wanajeshi? Huyo mpishi ndiye aliyepost picha za uchochezi mtandaoni?" Jimmy aliuliza huku nae wasiwasi ukimuingia,



    "Hawajasema ila walichoniambia ni kuwa ametumia mtandao kupotosha jamii" Mlezi wa kituo cha yatima aliongea,



    "Mambo yameharibika tayari, tuondoke" Gabby aliongea huku akinyanyuka, na wakaondoka hata bila kuaga na nje ya mlango waliweza kumkuta yule yule kijana ambaye ni Tom akiwa na dumu la mafuta ameliweka mabegani na shingo yake alikuwa ameiinamisha chini, wakampita na kupotelea getini.



    Tom akanyanyua shingo na kuwaangalia, akaweka chini dumu la mafuta na kukimbilia stoo, akachukua pesa yake anapoifichaga na kisha akabeba begi lake dogo mgongoni, aliamua kuondoka, aliamua kukimbia Mara baada ya kusikia maongezi kati ya wakina Gabby na mlezi wa kituo, kwa yale maelezo tu alihisi yeye ndio anayetafutwa kwa maana yeye ndiye aliyepost ile picha ya Waziri wa ulinzi na alihisi imeshaanza kuleta ukakasi ndani ya nchi, ila kilichomsaidia Tom ni kutumia simu isiyokuwa yake, alitumia simu ya mpishi na walichofanya vyombo vya usalama ni kufuatilia namba ya simu iliyotumika katika kuingilia katika mtandao huo wa kijamii.



    Tom akapita getini na begi lake na kuchukua bajaj na kupanda, hakuwa akijua ni wapi anapoelekea, alichokitaka ni kuondoka tu eneo hilo, alishaharibu tayari, hapakaliki tena, sio sehemu Salama kwa ajili ya usalama wake.



    *******************



    Koplo Mbegu alifika muda mchache tu baada ya Tom kuondoka, na yeye aliulizia ni wapi ilipo ofisi ya mlezi wa kituo na akaelekezwa, alienda na kukaribishwa na kisha akamsalimia mama yule mtu mzima,



    "Mama mimi ni polisi, kuna mtu namtafuta" Koplo Mbegu aliongea,



    "Sasa hivi wametoka wanausalama wengine, leo kweli mmeniamulia" Mlezi wa kituo aliongea kwa sauti ya upole,



    "Hao waliokuja walikuwa wanataka nini?" Koplo Mbegu alimuuliza,



    "Wanadai kuna mfanyakazi wangu amepost picha za kuposha jamii, nikawaambia ameshachukuliwa na wanajeshi tangu asubuhi" Mlezi wa kituo alijibu,



    "Kwa hiyo amechukuliwa na wanajeshi?" Koplo Mbegu aliuliza huku akishangaa,



    "Ndio wanajeshi tena walivaa magwanda, ila hawa waliotoka sasa hivi wamesema wametoka usalama wa taifa" Mlezi wa kituo alijibu,

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Dah, huyo kijana ni mfanyakazi wako wa muda mrefu hapa?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Sio kijana, ni mama mtu mzima kidogo, ni mfanyakazi wangu wa mwanzo mwanzo kabisa, ana miaka minne hapa" Mlezi wa kituo aliongea,



    "Mmama?" Koplo Mbegu aliuliza kwa mshangao,



    "Ndio, ni mama mtu mzima" Mlezi wa kituo alijibu,



    "Sasa mimi simtafuti huyo, namtafuta kijana wa kiume, anaitwa Thomas Anthony" Koplo Mbegu aliongea na kumfanya mlezi wa kituo ashangae,



    "Tom nae amefanyaje?" Mlezi wa kituo aliuliza,



    "Huyo ndiye alipost picha ambazo zinadaiwa kupotosha jamii na wala sio huyo mama aliyekamatwa" Koplo Mbegu alijibu,



    "Tom? Tom yupo, ebu twende tukamuangalie" Mlezi wa kituo aliongea huku akinyanyuka na kutoka nje ya ofisi huku akifuatwa na Koplo Mbegu.



    Walienda mpaka stoo ila hawakumkuta Tom, wakaelekea jikoni pia hawakumkuta Tom, safari yao ilipata jibu getini baada ya kuambiwa kuwa Tom ameondoka na bajaj na hakuaga ila alionekana akiwa na begi dogo mgongoni.



    "Tayari amekimbia, anajua ni yeye ndio anatafutwa" Koplo Mbegu aliongea huku akimuangalia Mlezi wa kituo cha yatima,



    "Huyu mtoto ana balaa jamani, mbona alivyokuja kuomba hifadhi alikuja kwa adabu na alionekana sio mtu mbaya?" Mlezi wa kituo aliuliza,



    "Ana akili sana, anajua kucheza na akili za watu, ni mbaya sana yule, kama akirudi toeni taarifa polisi, maana msipofanya hivyo mtakuwa mmejiweka matatani" Koplo Mbegu aliongea,



    "Tutatoa taharifa baba hata usijali" Mlezi wa kituo aliongea na Koplo Mbegu akaaga na kuanza kuondoka.



    Koplo Mbegu Alitoka nje ya geti na kuanza kutembea kwa mguu huku akifikiria namna Tom anavyocheza na akili za vyombo vya usalama, Kitu ambacho Koplo Mbegu hakukijua ni kuwa muda huo alikuwa anafuatiliwa na Gabby na Jimmy ambao wao baada ya kutoka ndani ya kituo kile walienda kutafuta chai na huko wakapata wazo la kuja kukaa maeneo yale huku wakisubiri kuona kama huyo mtu aliyechukuliwa na wanajeshi atarudishwa ili na wao wamchukue.



    Sasa wakiwa wanamsubiri ndipo walimuona Koplo Mbegu akiingia, wakapanga akitoka wamfuatilie, na wakati huu ndio Koplo Mbegu alikuwa akitoka sasa na wao ndio wakaanza kumfuatilia kwa akili sana, kwanza hawakuwa wakitembea kwa pamoja, waliachana kwa hatua si chini ya kumi na kila mmoja alikuwa akitembea upande wake wa barabara. Walifanya hivyo ili hata Koplo Mbegu atakapogeuka iwe ngumu kuwatambua kwa maana walishajua Koplo Mbegu anatembea kwa tahadhari sana.



    Koplo Mbegu aliendelea kutembea kwa muda huku akiwaza namna ya kuifuatilia hii kesi kwa maana kila siku ilikuwa inazidi kuwa ngumu.



    Koplo Mbegu akatoa simu yake na kumpigia simu mkuu wake na kumueleza hali aliyokutana nayo,



    "Kwa hiyo wanajeshi wamemchukua mtuhumiwa ila sio yule anayetakiwa?" Mkuu wa polisi aliuliza,



    "Ndio, ila mtuhumiwa nae amekimbia, na hajulikani alipo" Koplo Mbegu alijibu,



    "Ila nadhani kama jeshi imeamua kufuatilia basi ni jambo jema, kwa maana jeshi halipo upande wowote na hii inaonekana ni kesi ya kisiasa" Mkuu wa polisi aliongea,



    "Kwa hiyo unataka kusema ile kesi ya mauaji ya Rais na kuonekana kwa Waziri wa ulinzi wa zamani kuna uhusiano?" Koplo Mbegu alimuuliza,



    "Sijasema hivyo, wewe endelea kufuatilia kesi ya mauaji ya Rais" Mkuu wa polisi aliongea na kukuta simu na kumuacha koplo Mbegu akiangalia kioo tu cha simu yake.



    "Kama mnajua kila kitu ni kwanini unanisumbua?" Koplo Mbegu alijiuliza mwenyewe huku akiweka simu mfukoni.



    Hakutaka kuondoka mjini mapema kiasi hicho, alichofanya ni kuzunguka na kuchukua mahitaji yake kwa ajili ya nyumbani, alipanga arudi kijijini giza likiwa limeshaingia.



    Huku napo Gabby na Jimmy hawakuchoka kumfuatilia Koplo Mbegu, waliendelea kuzunguka nae kila mtaa, walichokuwa wanatafuta ni nafasi ya kuweka kumuua, ila hawakuweza kuipata kutokana na wingi wa watu maeneo yale ya mjini. Baada ya kuzunguka sana ndipo Gabby alipokea simu kutoka kwa Tammy Semmy, alitakiwa mmoja wapo aende ikulu mara moja, baada ya Tammy Semmy kukata simu, Jimmy na Gabby wakashauriana na mwisho wakakubaliana Gabby ndiyo aende ikulu na Jimmy aendelee kumfuatilia Koplo Mbegu.



    Gabby akaondoka na Jimmy ikaendelea kumfuatilia Koplo Mbegu kwa kila hatua anayopiga huku akiendelea kuwasiliana na Gabby.



    Mishale ya saa moja ilimkuta Koplo Mbegu akiwa kwenye bajaj akielekea kijijini, na Jimmy nae akachukua bajaj ambayo ilikuwa inaifuatilia kwa mbali ile bajaj aliyopanda Koplo Mbegu.



    Baada ya dakika Ishirini Koplo Mbegu alifika anapoishi kisha akashusha mizigo aliyokuja nayo na ikapokelewa na kijana mwenye maneno mengi,



    "Leo umeamua kushinda mjini" Kijana mwenye maneno mengi aliongea huku akibeba kiroba cha unga,



    "Kulikuwa na kazi kidogo, vipi biashara lakini?" Koplo Mbegu alimuuliza,



    "Namshukuru Mungu aisee, mzigo unatembea na faida naiona" Kijana mwenye maneno mengi aliongea,



    "Sawa, acha niingie nijipumzishe kama nusu saa, nitakuja baadae tupige story" Koplo aliongea,



    "Ungekula kabisa ndio upumzike, maana unaweza kushangaa unapumzika jumla mpaka asubuhi" Kijana mwenye maneno mengi aliongea,



    "Kuna chakula kumbe? chakula gani?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Ubwabwa na maharage tu" Kijana mwenye maneno mengi alijibu huku akicheka,



    "Basi ngoja nipumzike tu, lazima niamke nije nile kwa maana nina njaa" Koplo Mbegu aliongea huku akiingia chumbani kwake,



    "Sawa, mimi nipo nachambua chambua nguo za kuuza kesho" Kijana mwenye maneno mengi aliongea na kuingia ndani kwake.



    Jimmy alimwambia dereva bajaj aisimamishe bajaj mbali kidogo na aliposhukia Koplo Mbegu, kisha akamwambia dereva bajaj amsubiri na alimlipa pesa yake ya usafiri.



    Jimmy alisogea taratibu mpaka kwenye nyumba anayoishi Koplo Mbegu na alimkuta akiwa nje akiongea na kijana mwenye maneno mengi, akajificha kwenye kichaka na kusubiri kwa muda mpaka alipoona Koplo Mbegu ameingia chumbani kwake na kijana mwenye maneno mengi ameingia kwake.



    Jimmy akasubiri kwa dakika tano, kisha kwa mwendo wa kunyata akajisogeza mpaka kwenye mlango wa chumba cha Koplo Mbegu, akausukuma mlango na mlango ukakubali, Jimmy akajitoma ndani na kumkuta Koplo Mbegu akiwa anamuangalia huku akiwa amekaa, kutokana na giza lile, Koplo Mbegu hakuweza kumtambua mapema Jimmy mpaka jimmy alipojimulika na mwanga wa simu machoni,



    "Kumbe umehamia huku, ulijiona mjanja sana kutukimbia?" Jimmy aliuliza huku akitabasamu na kumfanya Koplo Mbegu ashtuke, maana hakitegemea ujio wa mtu yule usiku ule,



    "Nini hasa dhamira yenu?" Koplo Mbegu aliuliza huku akitetemeka,



    "Maswali sihitaji leo, maana unaweza kuniponyoka kama ulivyofanya mara ya mwisho" Jimmy aliongea huku akiielekeza bastola yake usawa wa kichwa cha Koplo Mbegu, na wala hakutaka kusubiri, alihiruhusu risasi kutoka na ukasikika mlio mkubwa mpaka majirani nadhani walisikia, Jimmy akatoa tabasamu.





    Jimmy alitoa tabasamu lisilo la kawaida huku bastola ikiwa mkononi na Koplo Mbegu akiwa mbele huku macho akiwa amefunga na pembeni yake ukutani usawa wa sikio kulikuwa na tundu la risasi lilitokana na risasi aliyopiga Jimmy kumkosa Koplo Mbegu na kutoboa ukuta, Koplo Mbegu aliisikia mlio wa risasi ila cha ajabu hakuhisi kuguswa na risasi yenyewe, akafungua macho na kumkuta Jimmy ameganda na mkono wa Jimmy ukalegea na kuachia bastola na akadondoka chini, nyuma ya Jimmy alikuwa amesimama Ghislain na bastola yake, yaani ina maana Ghislain ndiyo alimpiga risasi Jimmy na kufanya Jimmy apoteze shabaha ya kumlenga Koplo Mbegu na risasi ikampitia pembeni,



    "Umeniokoa rafiki yangu" Koplo Mbegu aliongea huku akiwa amekaa na alikuwa hana nguvu,



    "Hatari sana, ni nani huyu?" Ghislain aliuliza huku akiusogelea mwili wa Jimmy uliokuwa una tundu la risasi kwa kisogoni,



    "Mgeuze umtazame" Koplo Mbegu aliongea huku akiinuka na wakati huo Ghislain alikuwa akimgeuza Jimmy na pia kijana mwenye maneno mengi alikuwa anaingia ndani ya chumba cha Koplo Mbegu na alikuwa na wasiwasi sana,



    "Ah, huyu ni Jimmy, tupo nae usalama wa taifa" Ghislain aliongea baada ya kumgeuza Jimmy,



    "Watu watajaa sasa hivi hapa, ni nini kimetokea?" Kijana mwenye maneno mengi aliuliza,



    "Kazime taa chumbani kwako, funga na mlango kisha uje" Koplo Mbegu alimpa maelekezo kijana mwenye maneno mengi na kijana yule akatoka nje kwenda kufanya alichoagizwa.



    "Wewe umefikaje hapa?" Koplo Mbegu alimuuliza Ghislain,



    "Ni hadithi ndefu sana" Ghislain alijibu na wakati huo kijana mwenye maneno mengi alikuwa anaingia,



    "Nisimulie, maana nimepata mshangao" Koplo Mbegu aliongea,



    "Sisi ndio tulipewa jukumu la kumfuatilia huyo mtu aliyepost picha ya Waziri wa ulinzi, lakini tulipigiwa simu na jeshi kuwa hilo jukumu tuwaachie wao, tukakubali ila tukapanga twende maeneo yale ya kituo cha yatima ili tuangalie kuna nini kitatokea baada ya jeshi kwenda eneo lile, bahati nzuri wanajeshi waliondoka na mtuhumiwa vizuri tu bila kumpiga, sasa wakati nataka kuondoka ndipo nikamuona Jimmy na Gabby nao wakiingia eneo lile, nikashangaa wamefuata nini wakati tulishaambiwa usalama tusiusike tena na huyo mtu, nikaamua niendelee kukaa nje ili nijue ni kipi walifuata watu wale, mara nikawaona wametoka na wao wakaendelea kuwepo eneo lile, sikutaka kuwaonesha kuwa nipo hapo, niliendelea kubana sehemu huku nikiangalia nyendo zao, wakati nikiwafuatilia ndipo nikakuona na wewe ukiingia, nikajua utakuwa umetumwa na polisi, nikataka nikufuate ila nikasita kwa sababu sikutaka wakina Gabby wanione, baada ya muda nikakuona ukitoka, ulipoanza kuondoka nikashangaa Jimmy na Gabby wakikufuatilia, ikabidi na mimi niwafuatilie, mpaka walipoachana na mpaka Jimmy alipofika hapa na kutaka kukuua" Ghislain alimaliza kusimulia na kumuacha Koplo Mbegu mdomo wazi,



    "Asante, umeniokoa sana" Koplo Mbegu aliongea,



    "Kuwa mkweli sasa, ni kwanini hawa watu watake kukuua?" Ghislain aliuliza,



    "Kiukweli sijui, na hii ni mara ya pili wanafanya hili jaribio na ndio maana hata kwangu nimepahama na kuja huku kijijini" Koplo Mbegu aliongea,



    "Hawawezi kukosa sababu ya kuua, ebu kuwa muwazi" Ghislain aliendelea kudadisi,



    "Labda pengine ni dogo mmoja namfuatilia nahisi anahusika na mauaji ya rais, ila pia dogo huyo huyo ndiye aliyemuua Waziri mkuu" Koplo Mbegu aliongea,



    "Basi hiyo ndiyo sababu, kwa maana Jimmy na Gabby ni walinzi wa Tammy Semmy na inasemekana Tammy Semmy ndiye aliyehusika na kifo cha rais, kwa hiyo wanahisi wewe kumfuatilia huyo Dogo ni kwamba umeshajua siri yao" Ghislain aliongea,



    "Sasa kama mnajua Tammy Semmy ndiye aliyemuua rais wa hawali kwa nini hamumkamati?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Kuna njia na ushahidi wa kumkamata, huwezi kukurupuka tu kwa maana ana mtandao mkubwa na isitoshe sehemu kubwa ya usalama wa Taifa ni mtandao wake, ndio maana hata jeshi lilipoamua kuchukua kesi ya huyo mtu aliyepost ile picha ya Waziri mkuu kuna watu wa usalama wako hatarini kutokana na jeshi kutokuwa upande wa wowote na pia kama hujui ni kuwa huyo Waziri wa ulinzi ndiye aliyekamatwa kwa kosa la kutaka kupindua nchi na aliyekuwa nyuma yake alikuwa ni Tammy Semmy" Ghislain aliongea,



    "Tammy Semmy huyu Rais wa sasa hivi?" Kijana mwenye maneno mengi aliuliza,



    "Huyo huyo" Ghislain alijibu,



    "Lakini jeshi halijamkamata muhusika aliyepost hizo picha, wamemchukua mtu mwingine kabisa, aliyepost hizo picha ni Tom, kijana ambaye nimekueleza ndiye aliyemuua Waziri mkuu" Koplo Mbegu alieleza,



    "Tom mwenyewe yuko wapi?" Ghislain aliuliza,



    "Ndiye niliyemfuata pale kwenye kituo cha yatima, nikaambiwa ameondoka muda si mrefu" Koplo Mbegu alijibu,



    "Una ushahidi wa kutosha mpaka umuweke hatiani?" Ghislain aliuliza,



    "Ushahidi upo, huu hapa?" Sudy Bakari aliongea huku akiingia ndani na mkononi alikuwa na flash, Kijana mwenye maneno mengi alitaka kukimbia kwa maana alijua mtu huyo ameshakufa, kijana mwenye maneno mengi akakimbilia nyuma ya Koplo Mbegu na wakati Koplo Mbegu bastola ilikuwa mkononi kumuelekea Sudy Bakari, Ghislain alibaki anashangaa tu,



    "Vipi mbona sielewi?" Ghislain alijikuta anauliza,



    "Huyu naye ni muhusika wa mauaji ya Rais na Waziri mkuu" Koplo Mbegu alijibu huku bastola ikimuelekea Sudy Bakari,



    "Kiumbe mwenye akili finyu, unadhani ningewezaje kukuletea ushahidi kama na mimi ni mmoja wapo?" Sudy Bakari alihoji huku akimuangalia Koplo Mbegu,



    "Chukua hiyo flash na uipachike kwenye laptop yangu ipo ndani ya begi" Koplo Mbegu aliongea huku akimuangalia Ghislain ambaye alifanya kama alivyoagizwa, kisha akaitoa laptop na kuiwasha kisha akaipachika ile flash, tukio lililokuwa linaonekana ni lile la Tom kuonekana akimpiga risasi rais,



    "Umeipata wapi hii?" Koplo Mbegu aliuliza huku akimuangalia Sudy Bakari,



    "Umeamini ulichokiona? kama umeamini basi haina haja ya kunishikia bastola" Sudy Bakari aliongea na Koplo Mbegu akaweka Bastola chini,



    "Umepata wapi hii flash?" Koplo Mbegu alirudia swali lake,



    "Kiumbe unatakiwa ushukuru kwa msaada kidogo niliokupa" Sudy Bakari aliongea huku akitabasamu,



    "Naomba unisaidie kitu kingine, Tom yupo wapi?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Tom unamtaka wa nini?" Sudy Bakari aliuliza,



    "Ni mtuhumiwa wa mauaji, si hii flash yako inaonesha hivyo?" Koplo Mbegu aliuliza kwa ukali,



    "Ichunguze hiyo video kwa umakini, ukipata jibu nitafute" Sudy Bakari aliongea huku akiondoka, Koplo Mbegu akamnyooshea tena bastola,



    "Huwezi kuleta ushahidi alafu ukaondoka bila kutoa maelezo ya kutosha, rudi" Koplo Mbegu aliongea,



    "Kiumbe, hakuna mwanadamu wa kuniangamiza hapa kwenye hii mamlaka yenu, huo ushahidi unatakiwa ufanyie kazi" Sudy Bakari aliongea na kuondoka zake huku akimuacha Koplo Mbegu akiwa amenyooshea vile vile bastola yake,



    "Sudy huyu jamani, alishakufa na tulimzika, dah kweli dunia ina maajabu" Kijana mwenye maneno mengi aliongea huku akitoka nyuma ya Koplo Mbegu,



    "Huyu Jamaa aliyetoka hapa alishakufa? si ndio huyu nilikuchorea sura yake?" Ghislain aliuliza huku akimuangalia Koplo Mbegu,



    "Inasemekana alikufa, ila mimi nadhani anahusika na kifo cha rais" Koplo Mbegu aliongea huku akivaa shati lake,



    "Unatakiwa uhame hapa, sio Salama tena kwako hapa" Ghislain alimwambia Koplo Mbegu,



    "Watajuaje kama nipo hapa?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Kwa kutumia mtandao wa simu ya Jimmy, watagundua tu kwa maana mwili wake umekaa hapa muda mrefu" Ghislain aliongea na kufanya koplo Mbegu ampekue Jimmy na kuchukua simu yake kisha akakuta missed call tano zote zimetoka kwa Gabby,



    "Dogo inabidi uhame kwa muda hapa, mimi mwenyewe nahama ila sijui nitahamia wapi" Koplo Mbegu aliongea huku akiweka baadhi nguo kwenye begi,



    "Itabidi tukaishi wote kwangu, hili jambo linakaribia kufika ukingoni" Ghislain aliongea,



    "Sasa na hii maiti inakuwaje?" Kijana mwenye maneno mengi aliuliza huku akiuangalia mwili wa Jimmy,



    "Huyu tutaondoka nae" Ghislain alijibu na kufanya Koplo Mbegu amtolee macho,



    "Tunaenda nae wapi?" Koplo Mbegu aliuliza,



    "Tunaondoka nae, tutamtupa njiani, tukimuacha hapa itakuwa hatari zaidi" Ghislain alijibu,



    "Dogo chukua hii, hama hapa muda huu, tutakuwa tunawasiliana" Koplo Mbegu aliongea huku akimpatia pesa kijana mwenye maneno mengi, kisha akaweka begi lake mgongoni na kutoka nje huku akiwa amebeba Jimmy,



    "Kuna bajaj alikuja nayo Jimmy, itakuwa inamngoja" Ghislain aliongea huku akiongoza njia.



    Walipofika jirani na bajaj aliyokuja nayo Jimmy, ilibidi waufiche mwili wa Jimmy na kuisogelea bajaj, walipoifikia Ghislain akamtolea bastola dereva wa bajaj,



    "Unafanya nini sasa?" Koplo Mbegu akamuuliza kwa hasira Ghislain, maana hata yeye hakutegemea kama atatoa bastola,



    "Hivi vitu vinaenda na mipango" Ghislain aliongea huku dereva wa bajaj akitetemeka,



    "OK, ok tunafanyaje sasa?" Koplo Mbegu aliamua kukubali,



    "Mfunge kamba huyu" Ghislain alimwambia Koplo Mbegu na Koplo Mbegu akachukua kamba na kumfunga dereva bajaj kisha akamjaza vitambaa mdomoni na kumuweka siti ya nyuma ya bajaj, kisha wakaufuata mwili wa jimmy na kuna kuweka nyuma ya bajaj na koplo Mbegu akakaa nao, Ghislain ndio akawa dereva wa bajaj.



    Bajaj ilitembea mwendo mrefu kidogo mpaka ilipofika sehemu yenye kichaka na Ghislain akaisimamisha,



    "Tumtupie hapa" Ghislain aliongea huku akitelemka, kisha kwa kusaidiana na Koplo Mbegu, wakaushusha mwili wa Jimmy na kuupeleka ndani ndani ya kile kichaka na kuutupa, wakarudi kwenye bajaj na Koplo Mbegu akaingia ndani, Ghislain alisimama nje, alikuwa anajisaidia haja ndogo.



    Wakati Ghislain akiendelea kukojoa, kuna bajaj nyingine ikaja ikasimama hapo hapo, akashuka Gabby,



    "Vipi kamanda" Gabby alimsalimia Ghislain,



    "Poa, nambie Gabby?" Ghislain alijibu huku hofu ikimtawala,



    "Poa, mbona usiku usiku maeneo haya?" Gabby alimuuliza Ghislain,



    "Mida kama hii uwa naendesha bajaj yangu, si unajua hupaswi kutegemea mshahara tu" Ghislain alijibu,



    "Uko ulipotoka hujamuona Jimmy?" Gabby aliuliza,



    "Hapana sijamuona" Ghislain alijibu,



    "Una Wateja nini? nataka niambatane na wewe kwa maana inaonekana Jimmy ametekwa uko, ni bora niende na wewe mwenye mbinu za kivita" Gabby alimwambia Ghislain,



    "Nina Wateja aisee" Ghislain alijibu,



    "Si tuwafaulishe tu kwenye hii bajaj niliyokuja nayo, ngoja niongee nao" Gabby aliongea huku akielekea upande wa mlangoni mwa bajaj, Ghislain akapata hofu kuu.............





    "Au kama itawezekana ningoje hapa niwakimbize fasta, hawaendi mjini kabisa"Ghislain aliongea na Gabby akasimama,



    "Tatizo muda" Gabby aliongea,



    "Ila kwanini unahisi Jimmy ametekwa?" Ghislain alimtupia swali Gabby,.



    "Kuna mtu alikuwa anamfuatilia, tukawa tunawasiliana vizuri, ila muda huu ukimpigia simu yake inaita tu wala haipokelewi, napata wasiwasi" Gabby aliongea,



    "Jimmy kamanda wewe, hawezi kutekwa kizembe, labda anachofanya ni kuwa ameiweka silent simu ili ikiwa inaita isipige kelele kwa maana itawashtua watu anaowafuatilia" Ghislain aliongea,



    "Hilo unalosema inaweza kuwa kweli, ngoja mimfuate kwa maana natumia simu yangu kuangalia alipo yeye" Gabby aliongea kisha akarudi kwenye bajaj aliyokuja nayo na kupanda, akaondoka na kufanya Ghislain apande bajaj anayoiendesha na kuiwasha kisha akaiondoa, walikuwa wamenusurika mdomoni kwa Gabby,



    "Umejua nilikuwa naongea na nani?" Ghislain alimuuliza Koplo Mbegu,



    "Gabby, yaani huku nilikuwa nimeandaa bastola, angekuja tu nilikuwa namtawanya" Koplo Mbegu aliongea,



    "Anamfuatilia mwenzake, hii ni hatari sana kama tungeendelea kukaa pale, angetukuta huyu" Ghislain aliongea,



    "Sasa kama yule dogo hajaondoka pale mpaka muda huu, shauri yake" Koplo Mbegu aliongea baada ya kumkumbuka kijana mwenye maneno mengi.



    Bajaj ilitembea mpaka mpaka karibia na mjini, wakamtupa yule dereva bajaj, walimtupia jirani na barabara ili iwe rahisi watu kumuona, wenyewe wakaendelea na safari yao mpaka nyumbani kwa Ghislain kisha Koplo Mbegu akashuka na Ghislain akaiondoa bajaj, alikuwa anaenda kuiegesha kituo cha polisi, aliona ndio sehemu ambayo itakuwa Salama kwa bajaj na itakuwa rahisi pia kupatikana endapo dereva bajaj ataitafuta bajaj yake.



    *****"******************



    Gabby alivyoachana na Ghislain, alielekea moja moja kule kujijini huku akitumia simu yake kujua ni wapi alipo jimmy.



    Kwa kutumia simu yake aliweza kufika sehemu ambao bajaj haiwezi tena kuingia ndani ndani kutokana na wembamba wa njia, Gabby akashuka na kumwambia dereva bajaj amngoje hapo mpaka arudi.



    Gabby alitembea mwendo mfupi tu na simu yake ikamuonesha yupo jirani kabisa na alipo Jimmy, Gabby akazidi kusogea na uelekeo wake ulionesha jimmy yupo nyumba iliyopo mbele yake, ambayo ndio nyumba ya kijana mwenye maneno mengi na ndipo hapo Koplo Mbegu alikuwa akiishi.



    Gabby ikaendelea kunyata huku akiusogelea mlango ambao ulionesha jimmy yupo, mlango wa chumba cha Koplo Mbegu, alisogelea kwa mwendo wa kunyata, alipoufikia aliusukuma kwa nguvu na kuingia huku bastola ikiwa mkononi, ila hakukuta mtu zaidi ya simu ya Jimmy tu iliyokuwepo sakafuni na pia kulikuwa na damu chini. Gabby akaangaza hakuona mtu, akatoka nje pia akaangalia angalia ila hakuona mtu wala dalili ya kuwa na mtu,



    "Wamemteka" Gabby aliongea kisha akarudi ndani na kuchukua simu ya jimmy, kisha ile nyumba akaiwasha moto na kutoka zake nje, alikata tamaa ya kumuona Jimmy muda huo, aliamini kuwa Jimmy ametekwa tu.



    Gabby alirudi kwenye bajaj na kupanda,..



    "_turudi mjini" Gabby alimwambia dereva wa bajaj ambaye alitii na kuiondoa bajaj kwa safari ya kuelekea mjini, ndani ya bajaj Gabby alikuwa kimya, hakuongea neno lolote, alikuwa anafikiria ni kipi kimemkuta Jimmy mpaka akaiacha simu yake katika nyumba ile?



    Bajaj ilizidi kusonga tu mpaka muda huo tayari Gabby alikuwa amechangangikiwa juu ya hata ya Jimmy, ila hakuwaza kabisa kama Jimmy anaweza kuwa amekufa, alidhani tu inawezekana tu Jimmy ametekwa.



    Gabby alipofika mjini akashuka kwenye bajaj na kumlipa dereva na kisha akaenda sehemu moja ambapo magari huegeshwa kwa kulipia, kisha akaingia kwenye gari moja la kifahari, akatoa ufunguo mfukoni, akaliwasha na kuliondoa kwa mwendo wa kasi.



    Gabby aliendelea kuikimbiza ile gari huku kuna muda alikuwa akiongea mwenyewe, alifadhaika kutokana na kupotea ghafla kwa Jimmy.



    Safari ya Gabby iliishia ikulu, aliingiza gari moja kwa moja ikulu usiku ule. Gabby ni mtu aliyepewa Uhuru wa kuingia ikulu muda wote na ndio maana usiku huo mkubwa aliamua kwenda moja kwa moja ikulu.



    Gabby aliegesha gari yake na kushuka, kisha akawasilimia walinzi wachache wa ikulu na kuingia zake ndani, akapitiliza moja kwa moja kwenye chumba cha siri cha ikulu na kisha akampigia simu Tammy Semmy, alimtaharifu juu ya ujio wake.



    Baada ya dakika kumi Tammy Semmy aliingia kwenye kile chumba, alionekana ametokea kulala,



    "Mbona usiku huu, kuna habari gani mpya?" Tammy Semmy alimuuliza Gabby,



    "Jimmy haonekani, nahisi ametekwa na yule polisi aliyekuwa anamfuatilia mchana" Gabby aliongea huku akijikuna kichwa, hizo habari zilimshtusha Tammy Semmy,



    "Mbona hivyo jamani, huko jeshini sijui kinaendelea nini baada ya kumkamata huyo mtu aliyeeneza habari za Waziri wa ulinzi, na wewe tena unaniletea habari hizi, mbona hamfanyi mambo kiufanisi?, au mlilidhika tu pale nilipoapishwa?" Tammy Semmy aliuliza kwa ukali, nae alishachanganyikiwa,



    "Hii itakuwa mipango, kuna mtu nyuma ya hii" Gabby aliongea,



    "Yaani mpaka napata wasiwasi, watu wote waliokuwa kwenye mtandao wangu wanachunguzwa kimya kimya, simu zao zote zinafuatiliwa, upande wa jeshi hawaonekani kuwa upande wangu" Tammy Semmy alibwata,



    "Mkuu wa majeshi mtoe, muweke mwingine" Gabby alitoa ushauri,



    "Ndicho nilichopanga hicho, wiki ijayo nitamuweka mkuu mwingine wa majeshi" Tammy Semmy aliongea,



    "Jimmy sasa, hata sijui nifanyaje?" Gabby aliongea,



    "Nenda kapumzike Gabby, wewe ndio ngao yangu iliyobaki muda huu, Jimmy tutamtafuta kesho, nitakuongezea nguvu" Tammy Semmy aliongea huku akimpiga piga mabegani Gabby,



    "Sawa mkuu" Gabby aliongea huku akisimama,



    "Kama una shida nyingine niambie, au pesa zimepungua?" Tammy Semmy alimuuliza,



    "Hapana, pesa sioni faida yake tena, haya mambo yamenivuruga" Gabby alijibu, alishaona pesa changu, hazikuwa na maana tena kwake,



    "Sawa, kapumzike" Tammy Semmy aliongea, kisha Gabby akaondoka zake.



    "Yatapita tu" Tammy Semmy aliongea peke yake kisha akatoka katika kile chumba na kuelekea chumbani kwake kulala.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    *****************



    Ndani ya kambi ya jeshi, yule mpishi aliyekamatwa alifanyiwa mahojiano lakini alikataa kupost zile picha, alichosema ni kwamba kuna kijana mfanyakazi wa pale kituoni alimuazima simu yake kwa muda, huenda yeye ndiye alifanya hivyo. Wanajeshi wakarudi na yule mpishi pale kituoni lakini wakaambiwa huyo kijana waliyemfuata ambaye ni Tom, tayari ameshatoroka, mwanajeshi mmoja akaomba namba ya Tom anayotumia akiwa hapo, akapewa, kisha wakaondoka zao na kumuacha yule mama mpishi pale, ila walibeba simu yake kama ushahidi.



    Yule mwanajeshi aliyechukua namba ya simu ya Tom, alipofika ofisini kwao, aliiweka ile namba katika computer na kisha akabonyeza bonyeza na computer ikaonesha inatafuta kitu, baada ya nusu saa aliweza kukamata kila hatua ambayo Tom atapiga, uzuri ni kuwa kwa kile kifaa, hata Tom akizima simu bado kile kifaa kitamuonesha alipo, labda aitupe simu yake ndio itakuwa pona yake.



    Yule mwanajeshi kijana, mweupe na mrefu wa wastani akatabasamu,



    "Kazi ndogo hii" alijisemea huku akicheka, akanyanyuka na kuondoka zake, ilikuwa usiku, hakuwa na pa kwenda, alienda kulala.



    **************



    Asubuhi ilimkuta yule mwanajeshi yupo ofisini kwake, alikuwa bize akiangalia computer yake, alichokuwa anaangalia ni kile kifaa kinavyoonesha eneo Tom alipo, Yule mwanajeshi hakuwa na wasiwasi kabisa, kila muda alikuwa akiiangalia saa yake ya mkononi, ilipofika saa mbili Kamili asubuhi, alinyanyuka kitini na kuvaa kofia yake ya jeshi, kisha akaiseti simu yake na ikaanza kumuelekeza ni wapi Tom alipo. Mwanajeshi akatoka nje akachukua gari ndogo na kuanza kufuata maelekezo ya simu yake, baada ya nusu saa aliegesha gari nje ya mgahawa mmoja eneo la uswahilini, Tom alikuwa amekaa ndani ya huo mgahawa, alikuwa akipata kifungua kinywa, Mwanajeshi alipoingia akaenda kukaa katika kiti cha nyuma ya Tom, wakawa wamepeana mgongo,



    "Nipe maziwa fresh na chapati moja" Mwanajeshi aliongea huku akiiangalia simu yake iliyokuwa inamuonesha adui yupo nyuma yake.



    Akaletewa maziwa fresh na chapati, akaanza kunywa taratibu huku akiwa makini kumuangalia Tom, baada ya dakika tano Tom alimuita muhudumu ili amlipe,



    "Shilingi ngapi nadaiwa?" Tom aliuliza,



    "Mia saba tu" Muhudumu alijibu na Tom akaanza kujisachi, akatoa noti ya elfu kumi na kumpa muhudumu,



    "Harakisha chenchi" Tom aliongea na yule Dada akaenda kuangalia chenchi,



    Baada ya muda muhudumu alirudi,



    "Kaka chenchi nimekosa, hauna hela ndogo?" Muhudumu aliuliza,



    "Sina, nipe pesa yangu, nitawaletea baadae" Tom aliongea,



    "Utatuletea baadae vipi? Mtu mwenyewe hatukujui ndio tumekuona leo" Muhudumu aliongea,



    "Sasa tutafanyaje na mimi nina haraka?" Tom aliuliza,



    "Chukua hii, kata yangu na yake" Mwanajeshi aliongea huku noti ya elfu mbili ikiwa mkononi na alikuwa akimuangalia Tom huku akitabasamu,



    "Asante aisee" Tom alishukuru huku akitaka kuondoka,



    "Subiri, upo chini ya ulinzi' Mwanajeshi aliongea huku akiwa jirani kabisa na Tom, na muda huo alikuwa akining'iniza pingu mkononi, Tom akataka kukimbia alishtuka anapigwa mtama na kuanguka chini vibaya, yule mwanajeshi akatabasamu kisha akamsogelea Tom,



    "pole kwa kuanguka" Mwanajeshi aliongea huku akichuchumaa na kumfunga pingu Tom, ila sasa ile sura ya yule mwanajeshi haikuwa ngeni kabisa kwa Tom, hakujua aliwahi kuiona wapi? na wala hakuwa na kumbukumbu,



    "Broo niachie, mimi nakufahamu wewe" Tom aliongea huku akitaka kulia,



    "Umenijulia wapi?" Mwanajeshi aliuliza kwa dharau huku akitabasamu,



    "Sikumbuki vizuri, labda niambie jina lako, naweza kukukumbuka" Tom aliongea huku akiingizwa ndani ya gari, siti ya mbele, pembeni ya dereva,



    "Naitwa Joel Minja, ila wewe niite Sajenti Minja" Mwanajeshi alijibu na kuivua miwani yake nyeusi na kufanya jicho lake la kushoto lililokuwa na chongo lionekane vyema, akatabasamu kisha akawasha gari na kumfanya Tom amtolee macho tu........





    Kipindi chote hicho Tom alikuwa akitetemeka kwa maana aliamini kabisa mwisho wa mbio zake ndio umefika hapo, lakini kuna wazo lilimjia kuhusu Sajenti Minja, alijua kuwa huyu ndiye aliyeshughulikia suala la memory card mpaka mwisho, kwa hiyo Tom alijiaminisha kuwa huyu mtu ni mtu mwema, hayupo upande wa Tammy Semmy, ila sasa kitu alichojiuliza ni kwamba, mbona Edward Sambo nae alipigania suala la memory card lakini mwisho wake leo hii yupo upande wa Tammy Semmy? hata kama hayupo moja kwa moja basi anajua uovu wote wa Tammy Semmy.



    Japo Tom aliwaza hayo yote lakini aliona kukaa kimya ni ujinga, maana tayari ameshakamatwa na ni lazima apelekwe polisi tu, kitu ambacho Tom hakukijua ni kuwa alikamatwa kutokana na picha ya Waziri wa ulinzi, yeye alijua amekamatwa kutokana na mauaji ya viongozi wa nchi.



    "Lakini mimi sikuua, hata ushahidi upo" Tom aliongea huku akitaka kulia na kufanya Sajenti ashtuke ila hakuhuonesha mshtuko wake dhairi,



    "Ni nani sasa aliyeua?" Sajenti Minja aliuliza bila kujua ni kifo kipi anachokizungumzia Tom,



    "Ni BQ, ila nae alitumwa na Tammy Semmy" Tom aliongea,



    "BQ ndio nani?" Sajenti Minja aliuliza,



    "Ni yule Dada aliyekufa kwenye ndege jana, ndege iliyolipuka na Waziri wa ulinzi" Tom alijibu,



    "Kwa hiyo alitumwa kuua na Tammy Semmy?" Sajenti Minja aliuliza,



    "Ndio, hata kifo cha Waziri mkuu pia ni BQ aliua, alitumwa pia na Tammy Semmy" Tom aliongea na kufanya Sajenti Minja ashtuke sasa, maana hakujua ni vifo vipi vinaongelewa,



    "Sisi tunajua ni wewe ndio umeua, mara yako ya kwanza kuhusika na mauaji ulianza kumuua nani?" Sajenti Minja aliuliza kiakili ili Tom amtaje ni nani alimuua ambaye yeye anadai ametumwa na Tammy Semmy,



    "Si ndicho kifo cha rais nilichokuambia, alafu ndio kikafuata cha Waziri mkuu" Tom alijibu na kumfanya Sajenti Minja ashushe pumzi, maana hakutegemea kusikia habari kama hizo,



    "Sasa unavyokataa hujaua wewe na sisi tunajua wewe ndio muuaji, una ushahidi gani wa kukuepusha na hii kesi?" Sajenti Minja alimuuliza kwa lengo la kuendelea kumchimba,



    "Kuna video, anayo mtu mmoja hivi wa ajabu, jina lake simjui" Tom alijibu,



    "Anapatikana wapi na ana uhusianao gani na Tammy Semmy?" Sajenti Minja alimuuliza,



    "Hana uhusiano wowote na Tammy Semmy, ila hiyo video ambayo ndio ushahidi hata sijui aliipata wapi?" Tom alijibu wakati Sajenti Minja akiliegesha gari lake nje ya ofisi hapo kambini.



    Sajenti Minja akatelemka na Kisha akazunguka upande wa pili na kumfungulia mlango Tom kisha nae akashuka, akamshika mkono na kuanza kuingia nae ndani ya ofisi ya siri iliyopo hapo kambini, alimuingiza mpaka ndani na kisha akampigia simu mkuu wa majeshi na kumwambia habari hiyo ya kushtusha aliyoambiwa na Tom.



    Baada ya dakika kumi mkuu wa majeshi aliingia ndani ya ofisi hiyo ya siri na kumkuta Tom akiwa na Sajenti Minja, wakaanza kumuoji na Tom akaeleza mwanzo mpaka mwisho, hakuficha kitu kwa maana alijikatia tamaa.



    "Wasiliana na mkuu wa polisi na atupe namba ya polisi aliyepewa jukumu la kuifuatilia hii kesi" Mkuu wa jeshi alimwambia Sajenti Minja, Sajenti Minja akachukua simu yake na kumpigia mkuu wa polisi na kumueleza shida yake, Mkuu wa polisi akatoa namba ya Koplo Mbegu, hata hakusita kwa maana aliamini jeshi lipo kwa niaba ya nchi na wala sio kwa niaba ya watu fulani.



    Sajenti Minja alipokata simu aliyompigia Mkuu wa polisi, akampigia Koplo Mbegu na kumtaka afike muda huo makao makuu ya jeshi na aende na ushaidi wote alioukusanya ambao unahusu kifo cha aliyekuwa rais wa nchi.



    Koplo Mbegu alisita kutekelezo maagizo hayo kwa maana alihisi ni mtego wa usalama wa Taifa ili wamkamate yeye, lakini alikuja kukubali kwenda baada ya mkuu wake kumpigia simu na kumtaka aende Mara moja makao makuu ya jeshi.



    Koplo Mbegu hakubeba kitu chochote zaidi ya ile flash aliyopewa na Sudy Bakari, aliamini kule ndio ushahidi uliojitosheleza kwa sababu ni video zinaonekana na muhusika ambaye ni Tom ameonekana vizuri sana katika ile video.



    Koplo Mbegu akaenda mpaka makao makuu ya jeshi na akaelekezwa sehemu anapohitajika na kwenda moja kwa moja, ndani ya ofisi akamkuta Sajenti Minja, Mkuu wa majeshi na Tom.



    Koplo Mbegu akashtuka baada ya kumkuta Tom eneo hilo, hakutegemea kumkuta hapo. Koplo Mbegu akatoa heshima ya kijeshi kisha akapewa kiti na kukaa,



    "Wewe ndio ulikuwa unafuatilia mauaji ya kifo cha rais?" Mkuu wa jeshi alimuuliza Koplo Mbegu,



    "Ndio, ni mimi mkuu" Koplo Mbegu alijibu,



    "Mpaka sasa hivi umegundua nini juu ya kesi hiyo?" Mkuu wa jeshi aliuliza,



    "Kiukweli nimefanikiwa sana, hapa nilikuwa naangaika kumtafuta muuaji tu kwa maana sura yake ninayo na ushahidi akifanya mauaji ninao" Koplo Mbegu alijibu,



    "Muuaji ukimuona kwa sura unamtambua?" Mkuu wa jeshi aliuliza,



    "Ndio, ni huyo hapo" Koplo Mbegu alijibu huku akimnyooshea kidole Tom,



    "Mimi sijaua" Tom aliongea huku akitaka kulia,



    "Umesema ushahidi upo? ebu tuoneshe" Mkuu wa jeshi aliongea na Koplo Mbegu akaitoa ile flash mfukoni na kumkabidhi Mkuu wa jeshi. Moyo wa Tom ukapata mshtuko kwa maana flash iliyopo ni ile inayomuonesha Tom ndiye aliyesimama mbele ya kiti alichofungwa kamba rahisi.



    Mkuu wa majeshi akaipokea na kuweka kwenye computer iliyopo hapo ofisini ni ikaanza kuonesha tukio zima, kwa kweli ilikuwa ngumu Tom kujinasua kwenye lile tukio, kwa maana ni yeye ndiye aliyeonekana akimuua Rais.



    Tom alibaki analia tu kwa maana hakuona msaada wowote kipindi hicho.



    "Sasa huyu kijana anasema yote haya ni mipango ya rais wa sasa, ambaye ni Tammy Semmy, je kwenye uchunguzi wako umeona kuna kitu kama hicho?" Mkuu wa jeshi alimuuliza Koplo Mbegu,



    "Hapana, ila kuna wafanyakazi wawili wa usalama wa Taifa ambao inasemekana ni walinzi wa Tammy Semmy, hao naweza kuwahusisha" Koplo Mbegu alijibu huku akiwalenga Jimmy na Gabby,



    "Hao ndio wahusika wakuu, ila mimi mnanionea, Jimmy na Gabby ndio wahusika" Tom aliongea huku akitaka kulia,



    "Ila video inakuonesha peke yako, labda una video nyingine au picha ambayo inayoweza kuwa ushahidi?" Sajenti Minja aliongea huku akimuangalia Tom,



    "Kweli duniani hakuna haki, mnyonge muache anyongwe mpaka afe" Tom aliongea huku akilia,



    "Mmempataje huyu?" Koplo Mbegu alimuuliza Sajenti Minja,



    "Huyu tulikuwa tunataka tumuhoji kuhusu ile ishu ya kupost picha ya Waziri wa zamani wa ulinzi, lakini wakati nimemkamata tupo ndani ya gari ndio akaanza kuongea kuhusu masuala ya kuua, yaani amejikamatisha mwenyewe" Sajenti Minja aliongea na kufanya Tom ajione mpumbavu,



    "Sasa hapa nashindwa kumuweka Tammy Semmy hatiani moja kwa moja, kwa maana hatua ushahidi wa kutosha" Mkuu wa majeshi aliongea,



    "Ushahidi upo, tena umejitosheleza" Sudy Bakari aliongea huku akiingia ndani na kumfanya Koplo Mbegu ashangae na wakati huo huo Tom alitabasamu.



    Sudy Bakari akatoa ile flash ambayo inaonesha video anazoonekana Tammy Semmy na watu wake.



    "Sasa na hii nyingine inayomuonesha?" Sajenti Minja aliuliza,



    "Ngoja niwaoneshe" Sudy Bakari akaiendea computer ambayo ilikuwa na video ya Tom, akaiweka ikawa inaonesha kwa taratibu, yaani picha za mnato (slow motion) hapo ndipo ilipoonekana risasi ikipita pembeni ya Tom na kwenda moja kwa moja kwa rais. Wote wakashtuka,



    "Ni nani aliyerusha hiyo risasi?" Mkuu wa jeshi akauliza,



    "BQ" Tom akajibu haraka,



    "Ndio nani?" Mkuu wa jeshi akauliza,



    "Ndio huyu hapa" Sudy Bakari aliongea kisha akaifuata computer na kuinyooshea kidole, ghafla computer ikaanza kuonesha tukio la kuuawa kwa Waziri mkuu, tena mpaka BQ alionekana akiwa juu ya ghorofa, Sudy Bakari akaigandisha picha ya BQ na kuikuza, ikaenea kwenye kioo chote,



    "Nae yupo wapi huyu Dada?" Mkuu wa majeshi aliuliza,



    "Amekufa jana kwenye ajali ya ndege iliyomuua Waziri wa ulinzi" Tom akajibu na Sudy Bakari akatabasamu,



    "Sasa wamebaki wangapi?" Mkuu wa jeshi aliuliza,



    "Jimmy na Gabby" Tom alijibu,



    "Jimmy tumemuua jana" Koplo Mbegu akajibu,



    "Amebaki Gabby, anatakiwa akashikwe sasa hivi" Mkuu wa majeshi aliongea huku akimuangalia Sajenti Minja,



    "Nitampataje na sina namba yake na wala sijui anashindaga wapi?" Sajenti Minja aliongea,



    "Twende, mimi najua alipo" Sudy Bakari aliongea kisha wakatoka nje yeye na Sajenti Minja.



    "Huyu mtu ni nani, mbona ana miujiza hivi?" Mkuu wa majeshi alimuuliza Tom,



    "Mtu asiye na nguo" Tom alijibu huku akicheka na kipindi hicho ndicho Koplo Mbegu akawa anamuelezea mkuu wa majeshi kuhusu maajabu mengine zaidi ya Sudy Bakari.



    ****************



    Asubuhi ilimkuta Gabby akiwa ndani ya sebule ya ikulu na mbele yake alikuwa Tammy Semmy, walikuwa wakipata kifungua kinywa na muda huo pia walikuwa wakiangalia taharifa ya habari.



    Simu ya Gabby ikaanza kuita, alipoangalia jina la akaipokea ile simu,



    "Habari swahiba" Gabby aliongea baada ya kupokea simu,



    "Nzuri, kuna habari mbaya kidogo" Mpiga simu aliongea,



    "Habari gani tena swahiba?" Gabby aliuliza huku akionekana kushtuka,



    "Jimmy ameokotwa usiku wa leo akiwa amekufa, mwili wake upo Hospital" Mpiga simu alitoa habari iliyokuwa mbaya kuliko zote ambazo Gabby amewahi kusikia,.



    "Ana alama yoyote mwilini?" Gabby aliuliza,



    "Ana alama ya risasi kichwani" Mpigaji simu aliongea,



    "Sawa, nakuja hapo hospitali" Gabby aliongea kisha akakata simu na kumuangalia Tammy Semmy,



    "Vipi?" Tammy Semmy alimuuliza,



    "Jimmy amekufa, mwili wake umeokotwa njia ya kwenda kijiji cha gonge" Gabby aliongea huku sauti yake ikibeba hisia za uchungu sana,



    "Unasema?" Tammy Semmy aliuliza kama kwamba hajasikia alichoambiwa na Gabby,



    "Jimmy ameokotwa amekufa" Gabby aliongea,



    "Mungu nimekukosea nini? mbona watu wangu wanakufa hivyo?" Tammy Semmy aliongea kwa uchungu uku akiangalia juu,



    "Acha nikaangalie, nitakutaharifu" Gabby aliongea huku akinyanyuka kwenye kochi na kuondoka zake.



    Alielekea moja kwa moja hospitali ambao kweli aliuona mwili wa Jimmy na machozi yalimtoka, na aliamini kabisa aliyemuua Jimmy ni Koplo Mbegu.



    Gabby akatoa simu yake na kuwataharifu ndugu wa Jimmy juu ya tukio lililotokea, baada ya hapo alichukua gari yake na kuamua kuelekea eneo ambalo aliambiwa Jimmy ameokotwa.



    Alifika mpaka kwenye eneo hilo na kukumbuka hilo eneo ndilo walipokutana na Ghislain hapo, akahisi huenda Ghislain anajua kitu, akapanga kumchunguza.



    Gabby akageuza gari na kwenda moja kwa moja ofisi kwao, usalama wa Taifa, alipofika kitu cha kwanza alianza kumtafuta Ghislain, baada ya muda alimpata na kumtaka waende kwenye gari wakaongee, Ghislain alipata mashaka ila hakuwa na jinsi, akaenda kwenye gari na kuingia ndani,



    "Unajua Jimmy amekufa?" Gabby aliuliza,..



    "Nimesikia asubuhi hii" Ghislain alijibu,



    "Unajua sehemu aliyookotwa ndipo nilikukuta umesimama wewe jana?" Gabby aliuliza na moyo wa Ghislain ukazidi kwenda mbio,



    "Ndio, ila haimaanishi najua kuhusu kifo cha Jimmy" Ghislain alijitetea,



    "Na ile bajaj uliyokuwa unaiendesha jana unajua ipo polisi na dereva wake ameokotwa usiku wa jana?" Gabby aliuliza na Ghislain akashtuka zaidi,



    "Mimi sijui hilo" Ghislain alijibu,



    "Unajua kuwa maisha ya mtu mnafki ni mafupi sana?" Gabby aliongea huku akiichomoa bastola yake kiunoni na kumuelekezea Ghislain ambaye alibaki amekodoa macho huku akiwa hana la kufanya.......





    Kabla Gabby hajafanya kitu chochote alisikia mtu akigonga kioo cha gari na kumfanya aache kumfyatulia risasi Ghislain na kugeuka, kisha akateremsha kioo cha gari,



    "Nikusaidie nini?" Gabby aliuliza kibabe,



    "Naitwa Sajenti Minja, nimeagizwa kukuchukua na nikupeleke katika mahojiano maalum" Sajenti Minja aliongea kwa unyenyekevu,



    "Umeagizwa na nani?" Gabby aliuliza kijeuri,



    "Ni amri ya jeshi" Sajenti Minja alijibu,



    "Sawa nitakuja kwa muda wangu" Gabby alijibu huku akitaka kufunga mlango na pia alipata mshtuko baada ya kusikia ni amri ya jeshi, lakini kabla hajafunga mlango Sajenti Minja aliuzuia,



    "Natakiwa niondoke na wewe sasa hivi na sio baadae kama unavyosema" Sajenti Minja aliongea huku akiwa bado ameushika mlango wa gari ya Gabby,



    "Achia mlango huo, nimeshasema nitakuja baadae, usitake nikufanye vibaya muda huu" Gabby aliongea huku akiwa amepaniki,



    "Mlango nitauachia endapo utashuka ndani ya gari" Sajenti Minja aliongea huku akiwa ameung'ang'ania mlango wa gari,



    "Haujui unaongea na mtu mwenye cheo gani wewe, usajenti ni kinyesi tu kwangu, ebu acha mlango" Gabby aliongea kwa dharau,



    .



    "Siangalii pia wewe una cheo gani, hata ungekuwa rais bado ningekushurutisha ushuke" Sajenti Minja nae aliongea kijeuri baada ya kuona Gabby anamdharau,



    "Mpumbavu kumbe hunijui ee?" Gabby aliongea kwa hasira huku akishuka kwenye gari,



    "Sawa wewe unite utakavyo ila utaenda tu" Sajenti Minja aliongea huku akiachia mlango wa gari,



    "Unasemaje sasa" Gabby aliongea huku akimsukuma Sajenti Minja,



    "Hatujaja kupigana hapa, fuata maelekezo tafadhali" Sudy Bakari aliongea huku akitokea nyuma ya gari na kumfanya Gabby ashangae zaidi,



    "Kumbe na wewe ni mwanajeshi?" Gabby aliuliza huku akiwa na mshangao,



    "Kiumbe huna haki ya kulijua hilo kwa muda huu" Sudy Bakari aliongea huku akiichukua pingu kutoka kwenye mikono ya Sajenti Minja,



    "Unataka kufanyaje?" Gabby aliuliza,



    "Mimi sio kiumbe mfano wako, mimi ni kiumbe mfano wangu, hupaswi kuniletea pingamizi, weka mikono nikufunge pingu" Sudy Bakari aliongea huku akimtazama Gabby, ila Gabby hakuonekana kujali hilo, aligeuka na kutaka kupanda gari yake, Sajenti Minja akamvuta shati kwa nyuma na Gabby akageuka kwa hasira na kurusha ngumi nzito kumuelekea Sajenti Minja, ila kabla haijamfikia Sudy Bakari aliudaka mkono wa Gabby,



    "Hatujaja kupigana hapa, kiumbe kuwa mstaarabu" Sudy Bakari aliongea huku akimtazama Gabby,



    "Ebu niache wewe" Gabby aliongea kisha akarusha ngumi nyingine Kali kumuelekea Sudy Bakari, ila ile ngumi ikapita kama imepiga upepo,



    "Piga tena" Sudy Bakari aliongea huku akitabasamu, Gabby alirusha ngumi kama kumi na zote zilipita, na mwisho akaamua achomoe bastola yake, na kumuelekezea Sudy Bakari, kwa haraka sana Sudy Bakari akakipeleka kidole chake kwenye mdomo wa bastola na kuiziba,



    "Piga" Sudy Bakari aliongea huku akitabasamu na Gabby hakusubiri kitu, alifyatua risasi na ukasikuka mlio, kisha Sudy Bakari akatoa kidole na hakuonekana kudhulika kwa namna yoyote ile, Sajenti Minja akaendelea kushangaa maajabu ya Sudy Bakari,



    "Sasa zamu yangu kukupiga" Sudy Bakari aliongea na kisha kile kidole chake alichotumia kuuziba mdomo wa bastola akamuelekezea Gabby miguuni na kisha ikatoka risasi katika kidole cha Sudy Bakari na kumpiga Gabby miguuni, Gabby akaanguka chini kama mzigo,

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Nitashangaa sana kama utaendelea kushindana na mimi, maajabu mangapi nimekuonesha kiumbe?" Sudy Bakari aliuliza huku akimfunga pingu Gabby, na bila kutegemea Gabby alifyatua ngumi Kali na kumpiga Sudy Bakari shavuni, Sudy akamdhibiti na kumfunga pingu kisha akasimama na kumuangalia,



    "Wewe ni mwanadamu wa kwanza kugusa mwili wangu kwa pigo" Sudy Bakari aliongea huku akimuangalia Gabby kisha akatema mate yenye rangi ya njano.



    Baada ya hapo wakambeba Gabby na kumpakia katika gari waliyokuja nayo, kisha Sajenti Minja akakaa upande wa dereva na kuiondoa gari,



    "Hivi wewe ni mwanamazingaombwe?" Sajenti Minja alimuuliza Sudy Bakari,



    "Kwanini umeuliza hivyo?" Sudy Bakari aliuliza huku akitabasamu,



    "Una vitu Vingi sana vya tofauti na wanadamu wa kawaida" Sajenti Minja aliongea,



    "Ni kawaida tu" Sudy Bakari alijibu na kisha ukimya ukatawala mpaka walipofika katika kambi ya jeshi na kisha wakamshusha Gabby na kwenda nae mpaka kwenye chumba cha siri kwa ajili ya mahojiano.



    Walipofika walimkuta Koplo Mbegu, Tom na mkuu wa jeshi wakiwa ndani. Sajenti Minja akamsukuma Gabby na kuanguka chini kama mzigo,



    "Mkuu huyu ndo Gabby" Sajenti Minja aliongea,



    "Kijana unaweza kuniambia mahusiano yako na binti anayeitwa BQ?" Mkuu wa jeshi aliuliza huku akimuangalia Gabby,



    "Ndio mmenileta huku kwa ajili ya huu upuuzi?" Gabby aliuliza huku akimtazama Sudy Bakari,



    "Jibu swali wewe" Sajenti Minja aliongea huku akimtazama Gabby,



    "Nijibu nini sasa, hakuna chochote cha maana" Gabby aliongea huku akionekana ni mtu akiyekata tamaa,



    "Ushahidi upo, wala msiumizwe vichwa" Sudy Bakari aliongea kisha akanyooshea kidole computer moja na kisha kile kidole kikatoa mwanga na kule mwanga ukatua juu ya ile computer na ikaanza kuonekana video yote namna Gabby na wenzake walivyoanza kupanga mipango yote ya mauaji.



    "Hapo una cha kupinga?" Mkuu wa polisi aliuluza baada ya ile video kuisha,



    "Haina haja kumuhoji, nadhani ushahidi umetosha" Sajenti Minja aliongea,



    "Mpelekeni kizuizini kwanza" Mkuu wa polisi aliongea kisha Sajenti Minja akamchukua Gabby na kumpeka chumba maalum na kisha Sajenti Minja akarudi,



    "Na huyu naye bado ni mtuhumiwa, anatakiwa apelekwe kizuizini" Koplo Mbegu aliongea na kisha Mkuu wa majeshi akaamuru Tom apelekwe kizuizini kule alipopelekwa Gabby ila Tom asifungwe pingu kwa maana ametoa ushahidi wa kutosha.



    Sajenti Minja alimpekeka Tom kisha akarudi.



    "Nadhani wote tumeona ile video iliyoonesha mipango ilivyopangwa ya kifo cha rais na waziri mkuu, wahusika mmewaona na bahati nzuri na Tammy Senmy nae ameonekana na pia Tom alimtaja Edward Sambo kama ni mmoja wa watu wanaohijua hii siri ya kifo cha rais, sasa nenda na wenzako mkamkamate Edward Sambo, alafu mimi naenda kuitisha kikao mara moja" Mkuu wa majeshi aliongea kisha akaondoka na kuwaacha wakina Sajenti Minja wakijiandaa kwenda shirika la habari la Taifa kwa ajili ya kumkamata Edward Sambo.



    Walitoka wakiwa watatu yaani Sajenti Minja, Sudy Bakari na Koplo Mbegu. Wakachukua gari na safari yao iliishia katika shirika la habari la Taifa na wakaelekea moja kwa moja ofisini kwa Edward Sambo, na bahati nzuri walimkuta.



    "Minja mdogo wangu leo naona umenikumbuka" Edward Sambo aliongea kwa furaha,



    "Kweli ndugu yangu, ila huu ujio sio mzuri" Sajenti Minja alijibu,



    "Mbona unanitisha, kuna nini tena?" Edward Sambo aliuliza,



    "Unahitajika kwa mahojiano, kuna kesi inakuhusu" Sajenti Minja aliongea kwa utulivu,



    "Kesi gani?" Edward Sambo alihoji,



    "Utajua mbele ya safari, muda huu unatakiwa uongozane na sisi" Sajenti Minja aliongea na Edward Sambo hakuwa na swali jingine, aliweka vitu vyake saw a kisha akaambatana na wakina na Sajenti Minja.



    Walitoka nje na kuingia kwenye gari, safari ya makao makuu ya jeshi ilianza. Wakati wanatoka eneo la shirika la habari waliweza kupishana na magari kadhaa ya jeshi yaliyokuwa yanaenda shirika la habari, Sajenti Minja akatabasamu.



    "Mambo yameiva" Sajenti Minja aliongea huku akitabasamu na kufanya wenzie wamuangalie tu bila kutia neno.



    **********************



    Tom alipoingizwa chumba cha kizuizi alimkuta Gabby akiwa amekaa na pingu zake mkononi,



    "Dogo umeharibu maisha yangu, najua nitaenda jela, ila nikitoka uko lazima na wewe ufe" Gabby aliongea kwa hasira huku akitazama chini,



    "Nyie ndio mmeharibu maisha yangu, kwanza usiongee kitu" Tom aliongea kwa hasira,



    "Usiongee ujinga fala wewe" Gabby aliongea kwa hasira huku akisimama na mguu mmoja na kumfuata Tom, Tom akaona amechoka kufanywa mjinga, Tom alinyanyuka na kumsukuma Gabby, akakosa balance na kudondoka chini, Tom akamfuata na kuanza kumkaba kwa nguvu, Gabby hakuwa na la kufanya kwa maana mkononi alikuwa na pingu. Tom aliendelea kumkaba mpaka Gabby akaelegea, lakini Tom hakumuachia, alimkaba mpaka aliporidhika, alipomuachia Gabby akalala chini, hakuwa Gabby tena, ulikuwa ni mwili wake, Gabby alikufa mikononi mwa Tom.



    Tom hakulijua hilo alidhani Gabby amezimia tu, Tom akarudi kukaa sehemu yake huku akiwa bado na hasira.



    *************_****__



    Mkuu wa majeshi alikuwa ameshamaliza kufanya kikao cha dharula na viongozi wengine wa jeshi, na makubaliano waliyofikia ni kuipindua nchi, na muda huo alikuwa anaelekea ikulu kwenda kumkamata Tammy Semmy.



    Mkuu wa jeshi aliwachukua wanajeshi wachache ambao aliambatana nao mpaka ikulu, walipofika ikulu hawakupata upinzani kutoka wa walinzi wa Ikulu kwa maana walishapewa taharifa.



    Mkuu wa majeshi aliongoza mpaka nje ya ofisi ya Tammy Semmy na kuwakuta walinzi kadhaa wakiwa nje ya mlango wa ofisi ya Tammy Semmy,



    "Mlifanya nilichowaagiza?" Mkuu wa jeshi aliwauliza wale walinzi,



    "Ndio, tumemfungia humu ofisini kwake" Mlinzi mmoja aliongea kisha Mkuu wa jeshi na watu wake wakafungua mlango na kuingia, cha ajabu hawakumkuta Tammy Semmy, wote wakabaki na mshangao, isipokuwa mkuu wa majeshi, alibaki akitabasamu tu na kufanya vijana wake wamshangae....





    Wanajeshi wengine wakawa wanashangaa ni kwanini mkubwa wao acheke wakati Tammy Semmy haonekani, wakawa wanajiuliza au kafurahi Tammy Semmy kukimbia, au anajua ni wapi alipo Tammy Semmy?



    "Mkuu mbona umefurahi?" Mwanajeshi mmoja aliuliza,



    "Ebu sukumeni hiyo meza" Mkuu wa jeshi aliongea na wanajeshi wawili kati yao wakaisukuma ile meza, chini ya meza kulikuwa na kapeti la bei ghali ambalo lilitumika kutandikwa sakafuni,



    "Ondoa na hiyo kapeti" Mkuu wa jeshi aliongea na wanajeshi wakatii, kapeti ilipoondolewa kulikuwa kuna shimo,



    "Tammy Semmy atakuwa amekimbia tayari kupitia hili shimo, itakuwa vibaraka wake wameshampa taharifa juu ya tukio hili" Mkuu wa jeshi aliongea huku akitabasamu,



    "Kwani hilo shimo linatokea wapi?" Mwanajeshi mmoja aliuliza,



    "Limetokea uwanja wa ndege wa taifa" Mkuu wa jeshi alijibu,



    "Tupe agizo tuwahi uwanja wa ndege" Mwanajeshi mwingine alisema kikakamavu,



    "Nyie mnachotakiwa kukifanya ni kuikusanya familia yake ambaye ipo hapa ikulu na kuipeleka sehemu Salama" Mkuu wa majeshi aliongea huku akiitoa simu yake mfukoni na kumpigia Sajenti Minja, aliongea nae kwa muda mchache kisha akakata siku. Alimpa agizo la kwenda uwanja wa ndege na kuangalia kama ataweza kumuwahi Tammy Semmy au atapata habari yoyote kuhusu Tammy Semmy.



    "Nyie watatu nifuateni, natakiwa niende katika shirika la habari la taifa kwenda kutangaza mapinduzi" Mkuu wa majeshi aliongea na kisha akaelekea kwenye gari huku akifuatwa na wanajeshi aliowachagua na huku wale waliobaki wakikaa eneo la ikulu kwa ajili ya kuimarisha usalama.



    Mkuu wa majeshi akiwa na watu wake waliongoza moja kwa moja mpaka shirika la habari la utangazaji la taifa, walipofika walikuta wafanyakazi wote wakiwa wametolewa nje na eneo lote lilikuwa chini ya jeshi.



    Mkuu wa majeshi akaenda mpaka studio ya matangazo, kisha akaamrisha upigwe wimbo wa Taifa, baada ya wimbo wa Taifa kumalizika, mkuu wa majeshi alitangaza kuwa kuanzia muda huo nchi itakuwa chini ya jeshi la ulinzi na usalama, na akasema pia kuwa wananchi wataelezwa kila hatua na sababu zote za jeshi kupindua nchi.



    Baada ya hapo mkuu wa majeshi alitoka, na kurudi zake kambini kwa ajili ya kuongea na wanajeshi.



    **********************



    Sajenti Minja na wenzake walifika uwanja wa ndege na kuanza kukagua kila eneo lakini hawakuweza kumuona Tammy Semmy.



    Wakaamua waingie mpaka eneo la maulizo, walipofika wakauliza na kuambiwa ni kweli Rais Tammy Semmy alifika hapo na ameondoka muda mfupi uliopita, alipata ndege ya abiria iliyokuwa inaelekea urusi.



    Sajenti Minja akawasiliana na mkuu wa jeshi, na mkuu wa majeshi akamuamuru Sajenti Minja arudi kambini muda huo.



    kufikia hapo sasa Edward Sambo alishaelewa ni kitu gani kinaendelea ndani ya nchi.



    Sajenti Minja na wenzake wakarudi mpaka kambini na wakaanza kumuhoji Edward Sambo kuhusu anachokielewa kuhusu sakata hilo, akaeleza kila kitu bila kuficha, na hata alipotakiwa kuwataja wanamtandao wa Tammy Semmy aliwataja wote anaowafahamu yeye, na kila aliyetajwa alipokamatwa aliteswa na akawataja wengine, ndio ukawa mtindo huo mpaka wote waliposhikiliwa na wakafunguliwa kesi akiwemo Edward Sambo.



    Wote walihukumiwa kifungo cha miaka kumi gerezani ila Edward Sambo alifungwa miaka miwili kwa kuwa alikubali kutoa ushirikiano bila shuruti.



    Tom aliachiwa baada ya kuonekana hana kosa katika vifo vya rais na Waziri mkuu, ila kwenye suala la kifo cha Gabby alipatikana na hatia, akafungwa mwaka mmoja na nusu baada ya kusaidiwa kutetewa na jeshi na ikaonekana ameua bila kukusudia, ilielezwa alikuwa anakijihami baada ya Gabby kumshambulia.



    Koplo Mbegu, Sajenti Minja na Sudy Bakari walikuwa ni marafiki na kila mwisho wa wiki walikuwa wanaenda kuwatembelea Tom na Edward Sambo.



    "Sudy bado hatujajua hasili yako" Koplo Mbegu aliongea huku akicheka, walikuwa wapo nyumbani kwa Sajenti Minja ambapo ndipo Sudy Bakari alikuwa anaishi nae hapo,



    "Kiumbe utajua tu, hupaswi kuwa na haraka" Sudy Bakari alijibu, na ndiyo majibu yake ya kila siku pindi aulizwapo swali kama hilo.



    Walishazoeana wote watatu na walifurahi kutembea wote.



    ********************



    Tammy Semmy baada ya kufanikiwa kutoroka ikulu kwa njia ya handaki, alifanikiwa kulazimisha kupata ndege yoyote inayoondoka muda huo, na aliipata hiyo inayoelekea urusi, ikabidi abiria mmoja ashushwe ili mheshimiwa rais apate nafasi.



    Ndani ya ndege alikaa siti moja na mtu mmoja ambaye hakujua ni mwanamke au mwanaume, kwa maana alijifunika shuka ya kimasai karibia eneo lote la mwili na akaacha sehemu ndogo ya miguuni ambayo chini alivaa raba nyeupe zilizoandikwa "all stars"



    "Vipi unaelekea urusi ni kwenu au unaenda kwa ajili ya biashara" Tammy Semmy alimuuliza huyo mtu,



    "Ni mgonjwa, huyo anaenda kutibiwa maana aliungua na moto" mzungu aliyekaa pembeni wa huyo mtu alijibu, Tammy Semmy akashangaa kusikia Mzungu akiongea kiswahili vizuri hivyo,



    "Oooh wewe ni ndugu yake?" Tammy Semmy alimuuliza yule Mzungu,



    "Ni rafiki yake" Mzungu alijibu huku akitabasamu,



    "Huko urusi wewe ni mwenyeji?" Tammy Semmy alimuuliza,



    "Ni kwetu, hata huyu mgonjwa wangu ni kwao pia" Mzungu alijibu,



    "Oooh kwa hiyo nae ni Mzungu?" Tammy Semmy aliuliza huku akitabasamu,



    "Ni mzungu kiuraia, ila ni mtu mwenye asili ya kiafrika upande wa rangi" Mzungu alijibu,



    "Ni mvulana, maana sijajua" Tammy Semmy aliuliza,



    "Ni binti" Mzungu alijibu,



    "Basi akipona atakuwa mke wangu" Tammy Semmy aliongea kwa utani na wote wakacheka,



    "Usijali" Mzungu alijibu.



    "Nchini kwetu mlikuwa na biashara au mlikuja kutembea?" Tammy Semmy aliuliza,



    "Tulikuja kutalii ndio tukapata hayo matatizo" Mzungu alijibu,



    "Sasa mbona unaongea kiswahili vizuri kama umeishi sana?" Tammy Semmy aliuliza,



    "Nimejifunza, kabla ya kuja huku nilijifunza lugha yenu" Mzungu alijibu na kutabasamu.



    "Mama unaitwa nani?" Tammy Semmy alimgeukia mgonjwa aliyejifunika na shuka mpaka usoni na kuacha sehemu ndogo ya macho, lakini hakujibu na Tammy Semmy akaishia kutabasamu tu.



    Ndege ilipobakiza saa moja kufika Moscow, mji mkuu wa urusi, ilikuwa yapata saa nne usiku, Tammy Semmy alikuwa anasinzia, ndipo yule mgonjwa akajifunua shuka, Tammy Semmy ndipo alipomuangalia usoni, alishtuka, kwanza uso wa huyo mtu ulikuwa umeungua mpaka umeharibika, alikuwa anatisha, na pili hakuwa na mkono mmoja wa kushoto, ulikatikia chini ya kiwiko.



    "Pole sana" Tammy Semmy alimwambia,



    '"Asante, asante sana" Dada aliongea huku akitabasamu, lakini sauti yake haikuwa ngeni kwa Tammy Semmy,



    "Sauti yako sijui nimewahi kuisikia wapi? Umeshawahi kuwa mtangazaji" Tammy Semmy aliuliza,



    "Hapana, nimeshawahi kuwa mlinzi wako" Dada alijibu na Tammy Semmy akashtuka sasa, akataka kukurupuka ila alichelewa, Mzungu aliyekaa pembeni ya yule Dada aliruka na kuja kumziba na mto puani, na kisha yule Dada akatoa sindano ya sumu na kumshindilia Tammy Semmy kifuani, Tammy Semmy akatoa macho na nguvu zikawa zinamuishia taratibu.



    "Naitwa black Queen, naitwa BQ, nitarudi nchini kwako kuchukua mali ulizonipa" Dada ambaye ameungua uso na pia amekatika mkono mmoja aliongea na kutabasamu pamoja na yule Mzungu.



    BQ kumbe alikuwa hai, BQ hakufa kumbe, alipodondokea mtoni na ndege alijitahidi kuogelea ila mamba wakabaki na mkono wake, ila Waziri wa ulinzi aliliwa pia na mamba.



    Baada ya kumuua Tammy Semmy, BQ na yule Mzungu walimuwekea mto na kumlaza kwnye kiti na kumfunika na koti lake la suti usoni.



    Ndege ilipotua, BQ na yule Mzungu wakashuka na wakapotea eneo la uwanja wa ndege, wafanyakazi wa ndege waligundua baadae sana kuwa kuna mtu bado hajashuka kwenye ndege, na walipoenda kumuangalia wakakuta tayari ameshakufa muda mrefu tu, na walipoangalia passport yake wakagundua huyo mtu ni Tammy Semmy, ni rais huko nchini kwao.



    Walichofanya wafanyakazi hao ni kupeleka habari kwenye uongozi wao, uongozi ukawasiliana na uongozi wa nchi, uongozi wa nchi ukawasiliana na nchi ya Tammy Semmy na Urusi ikaambiwa huyo mtu anahitajika nchini kwake hata akiwa maiti.



    Urusi wakafanya mchakato na kuupakia mwili wa Tammy Semmy kwenye ndege ya mizigo ambayo ilikuwa inaelekea Kenya muda huo na mwili wa Tammy Semmy ukaondoka kurudishwa nchini kwake kwa njia ya ndege ya mizigo.



    Mwili ulifikishwa Kenya na kisha serikali ya Kenya ikautuma huo mwili mpaka nchini kwa Tammy Semmy na kisha ukapokelewa na jeshi, mwili uliharibika na ulikuwa unatoa harufu kutokana na sumu iliyotumika kumuua.



    Mwili ulikabidhiwa kwa mkewe na ukazikwa bila heshima yoyote ya serikali, ndio ukawa mwisho wa Tammy Semmy na jopo lake.



    **************************



    BAADA YA MIAKA MIWILI.



    "Mimi baadae naondoka, naenda kwetu" Sudy Bakari aliongea wakiwa sebuleni na Sajenti Minja, Koplo Mbegu, Tom, Edward Sambo na kijana mwenye maneno mengi ambaye alimsaidiaga Koplo Mbegu kipindi cha nyuma,



    "Baadae ya saa ngapi, maana sasa hivi ni saa kumi, au kwenu hakuna mabasi?" Sajenti Minja aliuliza kiutani na wote wakacheka,



    "Mtapajua baadae" Sudy Bakari alijibu,



    "Huyu mtu wa mazingaombwe bwana, anaweza kupotea tu akafika kwao" Koplo Mbegu akaongea na wakacheka.



    MISHALE YA SAA MBILI USIKU.



    Sudy Bakari aliwakusanya wenzake na kuwataka wachukue magari wamfuate, wenzake wakaingia kwenye gari ila yeye akasimama barabarani na kuanza kukimbia na gari walilopanda wenzake likawa linamfuata kwa nyuma.



    Walishangaa kuona anaelekea sehemu ambayo iliokotwaga maiti ya rais. Walienda mpaka kwenye lile eneo kabisa ambalo ndipo mwili wa rais ulifukiwa eneo hilo, wote wakawa na wasiwasi huku wasijue ni kitu gani anataka kukifanya Sudy Bakari kwa wakati huo.



    Sudy Bakari akasimama mbele yao,



    "Nawashukuru sana kwa muda wote ambao nimekaa na nyie, mnisamehe nilipowakwaza ila na mimi nimeshawasamehe mliponikwaza, Koplo Mbegu tumeshakwaruzana sana, ila hukujua kama mimi nipo upande wa haki, naitwa Dangudu, sio mwanadamu" Sudy Bakari aliongea kisha akanyamaza na kuanza kubadilika umbo lake na sura, akawa kiumbe cha ajabu sana, hapo sasa Koplo Mbegu na Ghislain wakakumbuka ule mchoro wao wa kitu cha ajabu waliouchora wakati wakianza upelelezi wa kifo cha rais.



    "Mimi ni kiumbe ambae naweza kujibadili sura na umbo lolote ninalolitaka, naweza kupotea na kutokea popote ninapopataka, nilichukua sura ya Sudy Bakari kwa kuwa alishakufa na pia sura yake na mwili wake ulikuwa shupavu, napenda mwanadamu shupavu mwenye uso wa kazi, ndio maana nitaendelea kumkumbuka Gabby kwa kuwa yupo hivyo pia, pia ni mwanadamu wa kwanza kunigusa kwa pigo.



    Tom ni mwanadamu wa kwanza kumuona nilivyokuja duniani, na ndio maana niliamua kumfuatilia na nikagundua ana matatizo, na nimemsaidia ingawa hakuwahi kuniamini" Sudy Bakari aliongea huku akiwa kwenye umbo lake la kutisha na wingu la mvua lilianza kutanda na radi na muungurumo vilianza kurindima eneo hilo, Sudy Bakari akaangalia juu na kisha akarudisha macho kwa wenzake,



    "Muda wangu umefika, muda wa kurudi kwetu, nitaweza kurudi tena duniani kama nitapewa ruhusa na baba yangu, mimi ni mtoto niliotokea katika uzazi wa utawala uko kwetu, hapa nilikuja kwa ruhusa ya kutembea na kujua mazingira ya wanadamu" Sudy Bakari aliongea na kucheka huku wenzie wakimuangalia kwa masikitiko,



    "Naweza kuwaachia utajiri wowote mnaoutaka ila sitoweza kufanya hivyo, nilivyokaa duniani nimegundua kuwa pesa na tamaa ndio chanzo cha kila kitu, ila nitakachowapa kama zawadi ni kimoja tu, hakuna mtu atakayelala na njaa na wala atakaye kuwa hana makazi kati yenu wote mliokuja hapa, ndani ya miezi mitatu yatatimia haya......mimi naenda, shikamaneni na mkatangaze upendo na mshikamano ndani ya nchi yenu yenye utawala mpya" Sudy Bakari aliongea na kutabasamu, kipindi hicho mvua ilishaanza kunyesha, Sudy Bakari akasogea mpaka katika kichaka kimoja, ambapo Tom alikumbuka kuwa hicho kichaka ndicho kilikuwa kinawaka moto kipindi anaufukia mwili wa rais.



    Sudy Bakari alipofika kwenye kile kichaka, alisimama na kunyoosha mikono juu, kisha akawaangalia wenzake na kutabasamu, kisha akarudisha macho juu na radi kubwa ikampiga na kumchukua na kupaa juu na kutokomea kusikokujikana huko angani, kile kichaka kikabaki kinawaka moto na Tom akatabasamu.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Watu wote wakatoka eneo lile kwa huzuni na kurudi kwenye gari na kuondoka zao kurudi majumbani kwao huku kila mmoja akimuwazia Sudy Bakari, maana alikuwa kama mwanafamilia kati yao.



    Na maisha mapya yalianza kwa Tom, maisha huru ndani ya nchi huru.



    **********MWISHO**********

0 comments:

Post a Comment

Blog