Search This Blog

Sunday 20 November 2022

URITHI WENYE UMAUTI - 4

 





    Simulizi : Urithi Wenye Umauti

    Sehemu Ya Nne (4)



    Jiwe moja ikanipiga kando ya sikio na kunisababishia maumivu yasiyomithilika.Hii ikanisababisha kuinama na kuruhusu mawe na vifaa vingine butu vilivyokuwa vinarushwa kwangu kukata hewa.Kuona vile nikachomoa bastola yangu kiunoni na kitendo kile kikawaogofya wale vijana wakaanza kusogea mbali kama mbwa koko.Sikutaka kuendelea kuwepo pale maana nilipoangalia nilipotoka nikawaona watu watatu,wawili wa kiume na mmoja wa kike wakija upande niliokuwa nikikabiliana na wale ombaomba.Nikajipenyeza kati ya vibanda vile na kuanza kutimua mbio za uhakika huku nikawa naviruka vidimbwi vya majitaka kimchezomchezo.Tayari mwili wangu ulikuwa umezoea sarakasi zile ngumu.Nilipofika eneo kulikokuwa kumejaa taka na mitungi mibovu ya plastiki,nilijificha pale na kutazama kule nilikotoka.Umbali ambao nilikuwa nimetoka ulikuwa mrefu sana.Nikawaona wale watu wakija upande ule lakini kwa taabu sana kwa kuwa walikuwa wakizama hapa na pale.Wote walikuwa na bastola mikononi ambazo sikujua miundo yake ni ipi maana zilikuwa ndefu kupita ile ambayo nilikuwa nayo.



    Niligeuza na kuendelea na safari yangu nikiwapuuzilia mbali wale watu.Akilini nikaanza kuhusisha tukio lile kwenye gereji nililotoka usiku ambako nilikumbana na mwanadada mmoja na mtu mwingine wa jinsia ya kiume wakiniwinda.Nao wale watu waliokuwa wakinifuata muda mfupi,kulikuwa na mwanadada ambaye alishahibiana na yule wa kule gereji akiitwa Ava ila wa kiume ndiye sikumkumbuka vyema.Wale watu kweli walikuwa na mtandao mkubwa sana.Safari yangu ikanifikisha kwenye eneo lenye biashara anuwai.Kulikuweko na akina mama wauza nyanya,mboga na matikiti huku wengine wakijihusisha na kuwakaanga samaki ambao walikuwa wakubwa.Upande mwingine wa barabara nikawaona wanaume wawili wakiwauza samaki wadogo wadogo waliokuwa wakijulikana kama 'omena'.Samaki hawa walikuwa wakitokea nchini Kenya Ziwa Victoria,Kisumu.



    Nikiwa nasomea shahada yangu ya uhandisi kule Uingereza,nilisikia tetesi kuwa kabila la Wajaluo ambao hujihusisha na biashara hii ya samaki 'omena' hawakuwauza kwa pesa.Tetesi zilidai kuwa wao(Wajaluo) hubadilisha samaki wale na ngono.Iliaminika kuwa wao walikuwa wakikubaliana na akina mama waliokuwa wakiwanunua samaki wale kubadilishana kwa njia ile.Dakika tano baadaye nikaona pahali ambako 'taxi' za kukodi zilikuwa zimepaki.Nilifululiza hadi pale ambapo kijana fulani mtanashati kati ya miaka thelathini akanipokea na kuniingiza garini."Dogo nikupeleke sehemu ipi maana naona umetokea CBD?"Yule kijana akaniuliza.Sikuwa na jibu la moja kwa moja hivyo nikamwamuru aendeshe tu nitamueleza.Haraka haraka nikawa nikifikiri pahali ambapo ningeelekea toka pale maana mji wa Sogomo ulikuwa haukaliki tena kwangu.Licha ya Hilo,nyumbani kwetu pia sikuwa na wakuishi naye maana watu niliokuwa nikiwategemea walikuwa wameangamizwa.Machozi yalianza kunibubujika mashavuni,sikujua hatima yangu ingekuwa vipi na wapi."Bratha mbona walia"ilikuwa sauti yake dereva wa 'taxi' lile iliyonishtua baada yake kunitazama."Hamna kaka.



    Nipo sawa tu"nilimjibu kwa kifupi."Mbona sijawahi mwona mtu aliyesawa akitiririkwa machozi?Kando na hayo unaonekana mwenye wasiwasi mwingi,kila muda mfupi watazama nyuma."Alisema dereva.Kwa kweli yule kijana alikuwa ameusoma mwenendo wangu vyema licha ya mimi na yeye kukutana kwa muda mfupi."Ni matatizo ya hapa na pale maishani"nikamjibu tena kwa kifupi."Matatizo gani yale?"Aliniuliza lakini nikabaki kimya.Maongezi Yale yalikuwa yameanza kuniudhi na kunichosha.Ukimya ukarudi tena mle ndani huku sauti iliyosikika pakee ikiwa ni mngurumo wa injini."Hujanieleza tunaelekea wapi"yule kijana akaniuliza."Mjini Kunaro"nikamjibu."Enhe!Kote kule muda huu?Huwezi kufika kule muda huu angalia hapa Ni saa kumi na nusu.Labda urudi mjini Sogomo uchukue chumba ulale usiku huu mpaka kesho"yule dereva akasema.Kweli alichokisema kilikuwa ukweli mtupu.Kufika mjini Kunaro ilikuwa ndoto ya mchana kutokana na muda kuwa umeenda sana."Sina hela zozote hata kidogo"nilidanganya.Dhamira yangu ilikuwa kufika kwa akina Sofia,mpenzi wangu."Na Mimi utanilipa nini maana tayari tumesafiri mbali sana toka mjini?"akaniuliza."Nilizobaki nazo"nikajibu."Ok turudi mjini.Nitakupa hifadhi kwangu usiku wa leo kisha kesho nitakuwahisha Kunaro"akasema kijana yule.Kiukweli nilifarijiwa na maneno yale toka kwa kijana yule.Moyoni nikajawa na furaha Kama kibogoyo aliyeota meno."Asante sana.Sijui nikushukuru vipi?"Nikamwambia."Huna haja maana wewe ni kama ndugu yangu licha yetu kukutana muda mfupi tu"akaniambia.Kwisha kukubaliana,aligeuza gari lile tukarudi mjini.Muda ulikuwa umesonga kwelikweli maana jua lilikuwa limeanza kuzama.Njiani tukawa tukipishana na magari mengi-si Lori,si mashangingi,yote yakiwa viashiria kuwa binadamu walikuwa wanaingia kwao,kupisha giza litawale.





    Tulichukua dakika ishirini hivi kufika alipokuwa akiishi yule kijana.Chumba alichokuwa akiishi kilikuwa cha kukodi.Kilikuwa na vyumba viwili,jikoni na chumba cha kulala,pia kulikuwa na kochi moja mle ndani lenye uwezo wa kuwabeba watu watatu tu."Karibu ndugu.Ila waitwa nani?"yule kijana akauliza.



    "Naitwa Roy,Roy Sikazwe"nikamjibu."Sasa Roy mimi ni Abdi Kanja.Naishi humu peke yangu hivyo kuwa huru"yule kijana,Abdi akasema.Nilimshukuru Abdi kisha nikajitupa kwenye lile kochi kwani uchovu ulikuwa mwingi.Abdi aliwasha jiko la mafuta ya taa na kuinjika sufuria alilokuwa ameweka mchele kisha akaanza kukatakata kipande kikubwa cha nyama ya ng'ombe."Je,taxi yako utaliweka wapi?"Nikamwuliza Abdi maana tulikuwa tumeliacha nje."Hukaa tu pale mpaka asubuhi.Hamna atakayeiharibu.Mbona kuna madereva wengi mtaa huu wanapaki yao mbele ya milango yao!"Abdi alinijibu.Chakula kilichukua muda mchache kuiva kisha Abdi akapakua kwenye sahani mbili huku akichanganya na ile nyama aliyokuwa amekaanga muda mfupi tu uliopita.Kwisha kula,tukaketi kochini huku tukipiga soga kuhusu mada ya hapa na pale.Kweli Abdi alikuwa muongeaji sana pia akiwa mjuzi wa mambo mengi.



    "Roy,uliniahidi kunielewesha masahibu yako.Huu ni muda mwafaka"Abdi akasema baada ya ukimya mrefu kati yetu kukatika.Sikuwa na budi,ikabidi nimsimulie yote yaliyonikuta.Nikaanza na historia yangu fupi ya masomo,kwa ujana wangu mpaka niliposafiri Uingereza kusomea uhandisi wa masuala ya kielectroniki.Kisha nikamsimulia jinsi niliporudi nyumbani kutokea jijini Kunaro kwa mpenzi wangu na kufika nyumbani kuwapata wazazi wangu wameuawa.Kweli nilipofika pale machozi yakanibubujika,Abdi akawa akinituliza kwa maneno yakuliwaza."Halafu ikawaje baada ya hapo?"Akauliza.Nikamweleza nilivyowatoroka wale watu kule nyumbani,Msituni Nyangumi hadi kwenye lile gereji nilikoponea chupuchupu kisha kule mapipani mpaka nilipoabiri taxi lake.Ilimchukua Abdi dakika tatu hivi kabla ya kuinua uso wake kunitazama.Alinionea huruma na kuniahidi kunisaidia katika kila hali."Pia Mimi nina simulizi inayoshabihiana na yako,ila nitakusimulia siku nyingine.Muda umesonga sana inatupasa tulale,kesho ni siku."Abdi akaniambia.Chumba chake Abdi kilikuwa kidogo ila iliyopangwa vizuri,kitanda kikubwa kikiipamba tokea katikati,nacho kikawa kimepunguza ukubwa mle ndani.Tukapanda juu na kujifunika blanketi kisha usingizi mzito ukanipitia.



    ****Niliamshwa na mtikiso wa Abdi akiniarifu kuwa muda ulikuwa umekwenda sana."Roy amka upate kiamsha kinywa.Tuna safari ndefu leo,angalia ni saa tatu kitambo"Abdi alisema.Niliamka na kuingia bafuni kisha nikakwenda kununua mswaki wa meno maana sikuwa nimesafisha meno yangu kwa muda na pia sikuwa nacho pale kwa Abdi.Kwisha maliza kupata kiamsha kinywa,nikajivika tena yale mavazi ya kikombati baada ya kutoa suruali fupi aliyokuwa amenipa Abdi.Kwa usiri nikaipachika bastola kiunoni na kuiteremsha shati,kuificha.Katika simulizi yangu sikuwa nimemweleza Abdi kuhusu ile bastola hivyo nikalazimika pia kutomweleza kuhusu yule mtu niliyemwua kule nyumbani.

    Muda mfupi baadaye,safari yetu kwenda mjini Kunaro ikang'oa nanga.fikra zangu zikaanza kuyarudia matukio yote ambayo yalikuwa yametokea tokea siku iliyopita.Maisha yangu yakawa yamegeuka shubiri.Ukimya ulikuwa umekita mle ndani, hamna aliyetamka chochote.Tulipishana na magari tofauti tofauti,mengine yakielekea mjini Sogomo tulikokuwa tukitokea huku mengine yakitupita.Kwa kweli hali ile ya yale magari ikawa ikinipa funzo fulani maishani.Kwenye maisha watu huwa tofauti Kama magari;kuna wale wanajaribu kufa na kupona kufika ulipokuwa huku wengine waking'ang'ania kukufikia ulipo hata kukupita ulipo.

    Tulifika Kunaro saa sita mchana.



    Biashara kadha wa kadha zilikuwa zikiendelea,kila binadamu akiwa kwenye hamsini zake.Wachuuzi wa karanga na soseji walikuwa wakijaribu kuwauzia abiria waliokuwa wameketi karibu na madirisha ya magari.Hatukupata usumbufu mwingi maana Abdi alikuwa akiendesha gari mbio huku tukisimama pahali palipokuwa na mikusanyiko ya watu.Tuliwasili katikati ya mji Kunaro saa sita na nusu mchana.Tulifululiza mpaka chuo kikuu cha Romi ambako alikuwa akisoma Sofia.Sikumjulisha ikiwa ningefika pale siku hiyo maana tangu nigundue kuwa wale watu walikuwa wakinifuata kwa kufuata mawimbi ya mawasiliano ya rununu yangu,nikachukua uamuzi wa kutoifungua kamwe.Tulipita kwenye lango kuu mpaka zilipokuwa hosteli za wasichana.Kwa vile nilikuwa nikijua chumba alichokuwa akiishi mpenzi wangu,tukafululiza naye Abdi mpaka kule.Hakukuwa na idadi kubwa ya wanafunzi mle ndani maana wengi wao walikuwa wamekwenda kusoma vipindi vya mchana.Sofia alikuwa anasomea udaktari mwaka wa tatu.Tulifikia mlango nambari sitini(60) alikokuwa akiishi Sofia.Ndani kulisikika mziki hafifu wa 'R n B',aina ya mziki ambao ulisadikika kuwa ulianzishwa na wazungu weusi mwaka wa 19''.Muziki uliendelea kuimba tukikaribia chumba hicho.Sofia alikuwa amenizoesha kuingia mule chumbani bila ya hata kupiga hodi.Kweli tulikuwa tumeelea kwenye penzi zito,tukawa kama upinde na mshale au tuseme ulimi na mate.Niliusukuma mlango na kuingia,Abdi akinifuata nyuma.***Picha niliyoikuta mle ndani,ikaufanya moyo wangu nusura unipasuke.Juu ya kitanda kulikuwa na miili miwili,zikiwa kwenye penzi zito.



    Sofia alikuwa amefunga macho huku akihema polepole ikawa nimepata jibu la mziki ule kuwekwa kwa sauti hafifu.Yule Mwanamume sikuweza kumtambua mara moja maana alikuwa amelala kifudifudi huku Sofia akiwa kingalingali.Abdi alisimama kando yangu,akiwa ameachama mdomo.Kweli hakukuwa na kiungo chochote mwilini mwangu ambacho kilikuwa radhi kusonga hata sentimita chache.Dakika chache baadaye,Abdi alisogea mpaka ilipokuwa redio ile Kisha akaizima kabisa.Kitendo kile kiliwashtua sana Sofia na yule mchepuko wake,mshangao niliouona usoni mwa Sofia ulikuwa wa kuogofya."Bebi mbona umeshtuka"yule mwanamume akamwuliza Sofia maana yeye hakuwa ameusoma mchezo.



    Lile likawa pigo la pili kwangu baada ya lile la kuuliwa kwa wazazi wangu.Hii leo mtu niliyekuwa namwamini alikuwa amenisaliti.Hasira ilikuwa ikinipanda,nikaangalia chumbani mle kifaa chochote nimwadhibu yule baradhuli sawasawa.Yule mwanamume alipogundua kilichotokea akaruka juu kama mtu aliyeingiwa na pepo.Sehemu yake ya siri ikawa ikinyong'onyea haraka ungedhani ni mmea kifaurongo."Baby,nini hiki?Nani hawa?"Yule mwanamume akamwuliza Sofia.Muda wote huo, Sofia alikuwa amejikunyata pale kitandani akiniangalia,mkono mmoja mdomoni mwingine akijaribu kujisitiri,machozi yakimtiririka.Abdi naye alikuwa amesimama palepale ilipokuwa redio ile,akitazama mchezo wote ulivyokuwa ukijianika mbele ya macho yake.



    "Sofia sababu ya haya yote ni nini?"Nikamwuliza Sofia ila akashindwa kunijibu.Muda mchache,yule mwanamume akashuka kitandani na kuvaa suruali yake ila kabla ya kuvaa shati lake,nikapata wazo.Nikakumbuka kuwa kiunoni nilikuwa nimebeba ile bastola ya wale watu.Haraka nikaichomoa.Kitendo kile kikawashangaza wote mle ndani.Abdi naye hakuamini kile alichokiona mbele yake,naye alikuwa katika hali ileile ya Sofia na mchepuko wake.Yule mwanamume alikuwa akitetemeka mwili wake wote."Lala kwenye sakafu mara moja"nikamwamuru,naye bila hiyana akatii.Akalala kifudifudi huku jasho likianza kumtiririka mgongoni.Nikamsongea Sofia pale kitandani,kisha kwa nguvu nikamnasa kibao,kilichombamiza ukutani huku ukemi ukimtoka.Nikamfuata na kumziba mdomo ila nilipogundua bado sauti ya kilio kilikuwa kikimtoka,nikachukua chupi yake na kuisokomeza mdomoni kisha nikamwinua mpaka kwenye kiti kilichokuwa mle ndani.Nikachanua shuka na kumfunga mikono na miguu.Dozi sawa ikafuata kwa yule mwanamume ambaye nilimfunga kwenye meza ndogo ya kusomea miguu yake ikawa ikielea.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog