Search This Blog

Friday 18 November 2022

SALA YA SARAH - 3






Simulizi : Sala Ya Sarah

Sehemu Ya Tatu (3)







Sarah alipofika kwenye gari yake aliingia na kufungua eneo la mbele na kutoa dawa, akachukua pamba na kuanza kuipaka kwenye eneo la shingoni na kichwani juu ya sikio ambalo alijeruhiwa na Aisha.



Sarah alipomaliza kujipa huduma ya kwanza, aliwasha gari lake na kuondoka, alikuwa anarudi kwake,



"yule mwanamke ni nani?, alafu ametumwa na nani?" Sarah alijiuliza wakati akiendesha gari yake,



"hii vita inaanza kuwa nzito, maana wanaingizwa wapambanaji, tena wenye uwezo mkubwa" Sarah aliongea huku akimfikiria Aisha namna alivyomdhibiti kiurahisi.



Sarah aliingia nyumbani kwake huku akiwa na hasira, alipofika sebuleni hakutaka hata kupoteza muda, alivua viatu tu na kisha moja kwa moja na kuelekea kwenye chumba cha siri, huku mkononi akiwa amebeba chakula kwa ajili ya mjomba wake, bwana Taita.



Alifika ndani ya chumba na kuwasha taa, Taita alikuwa amelala sakafuni huku akiwa bado amefungwa kamba,



"Sarah hivi si uniachie tu, umetaka hela nimekupa, lakini huniachii, kwanini?" Taita aliuliza kwa upole,



"hela yako naweza kukurudishia, tatizo sio hela, suala la kukuachia ni mimi mwenyewe nikiamua na wala sio pesa yako" Sarah alijibu huku akimfungua Taita ili ale chakula alichomletea,



"basi kama tatizo sio pesa, niache nikafanye shughuli zangu, biashara zangu zinakwama uraiani" Taita aliongea kwa kulalamika,



"ngoja nikuulize kitu, hivi Katika kambi yenu kuna mwanamke hata mmoja?" Sarah alimuuliza Taita,



"mwanamke????? Hapana" Taita alijibu huku akifakamia chakula,



"kuna mwanamke alinivamia leo na kudai ametumwa, sasa ametekwa wapi huyo mwanamke?" Sarah alimuuliza Taita,



"Mimi sijui kwa kweli, kwani wewe unapambana na maadui wangapi?" Taita aliuliza,



"sina adui mimi" Sarah alijibu,



"sasa kama huna adui si uniachie" Taita aliongea,



"nitakuachia, ila siku ninayokuachia itabidi na babu yangu na mwanae wawe huru" Sarah aliongea,



"mbona baba mdogo alishaachiwa, ila babu yako ndio bado" Taita aliongea kwa kujiamini,



"sawa kama mmemuachia, ila mimi shida yangu ni babu" Sarah aliongea,



"nipe simu niwaambie wamuachie" Taita aliongea,



"hupaswi kuwa na haraka, hii shughuli ina utaratibu wake" Sarah aliongea huku akisimama,



"mama mbona unaondoka? Ina maana ndio na leo huniachii?" Taita alilalamika wakati Sarah akitoka, ila leo hakutaka kumfunga Taita Mikono, alimuacha huru tu.



Sarah akaenda sebuleni na kumpigia simu Harry,



"Sarah naongea" Sarah alijitambulisha baada ya Harry kupokea,



"nakusikilza" Harry alijibu huku akipata hofu,



"kesho kutwa naomba tuonane, kuna kitu nataka unisaidie" Sarah aliongea na kufanya Harry ajiulize ni kweli Sarah anahitaji msaada au mtego,



"sawa, tutaonana wapi?" Harry aliuliza,



"sema wewe, nitakuja popote kwa kuwa nina shida" Sarah aliongea kwa utulivu,



"ok, tutakutana Vin hotel, saa mbili usiku" Harry aliongea,



"na iwe hivyo, usiniangushe mwanasheria" Sarah aliongea,



"usijali" Harry aliongea kisha Sarah akakata simu, akatabasamu,



"wewe si ni mwanasheria? Utanisaidia kesi yangu sasa" Sarah aliongea peke yake kisha akatupa simu mezani.



*******************



Siku nyingine tena, Aisha alikutana na Harry katika mgahawa ule ule waliokutana hawali,



"nilikutana na msichana wako, nimemjaribu kabisa, ni mwepesi mno, basi tu sikutaka kumuua" Aisha aliongea huku akitabasamu,



"Sarah??" Harry aliuliza,



"ndio huyo huyo, hana lolote mpaka nikahisi pesa yako naila bure tu, maana hata kupambana hawezi" Aisha aliongea kwa dharau,



"huyo atakuwa sio yeye, ulipambana na mwingine" Harry aliongea huku akiwa haamini,



"kama huamini sawa, ngoja muda ufike tu" Aisha aliongea,



"sasa kwanini hujamuua?" Harry aliuliza,



"uwa siui mpaka malipo yakamilike" Aisha alijibu,



"ungeua tu, au hatuaminiani?" Harry aliuliza,



"kazi haramu hazihitaji kuaminiana" Aisha alijibu,



"sawa, ila sasa tayari nimeshakamilisha malipo yako, na kama utaweza leo usiku anza kazi, nitakutana mahala na Sarah, anadai anataka tuongee" Harry aliongea,



"haina shida, kwa kuwa malipo umekamilisha leo, basi na kazi itaisha leo" Aisha aliongea kwa kujiamini,



"basi sawa, saa mbili usiku nitakuwa nae Vin hotel, uje pale" Harry aliongea,



"nitakuja ila hatutaonana, nitaweka mitego yangu" Aisha aliongea,



"poa, basi baadae, acha niwahi kazini" Harry aliongea huku akisimama na Kuondoka zake, akamuacha Aisha akiendelea kupata juisi.



**************



Mishale ya saa mbili usiku, Sarah akiwa amevaa suruali nyeusi na koti la suti lenye rangi ya njano isiyokoa, alikuwa akiingia pale Vin hotel, alielekea moja kwa moja sehemu ambapo Harry alikuwa amekaa,



"shikamoo" Sarah alimsalimia Harry wakati akikaa,



"marhabaa, Harry aliitikia huku akikishangaa kisarah kilivyo kidogo alafu kinawaendesha,



"bila kupoteza muda, nimekuja kwa jambo moja hapa, nataka nifungue kesi ya mauaji dhidi ya Taita, naomba uwe wakili wangu" Sarah aliongea huku akimtazama Harry, hiyo kauli haikumshangaza tu Harry, ila ilimtisha kabisa, maana alijua kabisa yeye ni mtuhumiwa wa hiyo kesi pia,



"mauaji ya nani?" Harry alituliza akili kisha akauliza,



"vifo vya wazazi wangu" Sarah alijibu na kumuona namna Harry alivyoshtuka,



"hiyo haiwezekani, kama huna cha maana kilichokuleta bora uende tu" Harry aliongea kijeuri,



"kwa hiyo hilo sio la maana?" Sarah aliuliza huku akitabasamu,



"naona huna jipya, siku ukiwa na cha maana utaniita tena" Harry aliongea kijeuri huku akinyanyuka na kuondoka, alijiamini na pia aliamini Sarah hana muda mrefu wa kuishi.



Harry alitoka na kupanda gari yake, akaondoka. Baada ya dakika tano za kuondoka Harry, Sarah alitoka Vin hotel, siku hakuwa na gari, akawa anatembea huku akiamini anaweza kupata bajaj.



Alitembea mwenda mrefu bila kuona bajaj wala boda boda, na kumbuka Vin hotel ilijengwa nje ya mji. Sarah akiwa eneo ambalo kuna miti mingi, ndipo alipoweza kumuona mtu akija nyuma yake, kwa kuwa kulikuwa na giza basi ilikuwa ngumu kumtambua huyo mtu.



Yule mtu akazidi kupiga hatua mpaka akamsogelea Sarah,



"tumekutana tena kwa mara nyingine mrembo" Aisha aliongea na kufanya Sarah amkumbuke, Sarah alishtuka sana,



"ulikuwa unanitafuta, bado hujaridhika na ulichonifanyia?" Sarah alimuuliza,



"nilikuwa sijalipwa, ila leo nimelipwa na nimekuja kuhitimisha kazi" Aisha aliongea,



"hitimisha tu, ruksa" Sarah aliongea na kumfanya Aisha aanze kumsogelea kishari, kwa kujihami Sarah akamrushia ngumi za haraka haraka, Aisha akarudi nyuma, Sarah akamrukia na teke likamkuta Aisha kifuani, akadondoka na kunyanyuka, Sarah akarusha tena ngumi mfululizo, Aisha akarudi nyuma akajikuta ameingia kwenye miti, Sarah akamuendea kasi na kurusha ngumi nyingine, Aisha akamdaka na kuachia kifuti kilichomkuta Sarah tumboni, Sarah akagugumia kwa maumivu,



"wakati unarusha ngumi zako sio kwamba nilikuwa naziogopa, nilitaka nikuvutie huku porini ili nikumalize bila shida" Aisha aliongea kwa dharau, kisha akaachia ngumi mfululizo zilizomkuta Sarah shingoni, Sarah akaenda chini,



"nyanyuka tuendelee" Aisha aliongea huku akizitoa pingu zake mfukoni, Sarah akanyanyuka na kurusha teke kali, Aisha akaudaka mguu wa Sarah kisha akautupa kiufundi, Sarah akajikuta anazunguruka, Aisha akaudaka mkono wa Sarah na kuufunga pingu, Sarah akaona akilegea ataumia, akarusha ngumi kwa ule mkono wake uliobakia, Aisha akainama na kuushika, akautia pingu na ule mkono kisha akamvuta Sarah kwa nyuma na kumtia kabali, Sarah ujanja ukaisha,



"bado sana katika masuala ya kupambana, nenda kajifunzie kuzimu" Aisha aliongea huku akitabasamu na kuchomoa kisu chake, akakipeleka shingoni kwa Sarah, Sarah akataka hata kukurupuka, ila alishindwa, alibanwa kiufundi haswa, kwa mara ya kwanza machozi yakamtoka Sarah katika pambano, hakuwa na msaada ingawa aliuhitaji sana kwa muda huu...........









Wakati Aisha akikipeleka kisu shingoni kwa Sarah, ulisikika mlio wa bastola, Aisha akageuka nyuma na kumuona mtu akiwaendea kwa kasi huku akiwa na bastola mkononi, Aisha akaona bora amalize kazi haraka kabla huyo mtu hajawafikia, Aisha akanyanyua kisu juu ili amchome nacho Sarah shingoni, wakati kisu kikiwa juu, kilipigwa na risasi na kile kisu kikadondoka chini, Aisha akatoa tusi la nguoni kumuelekea yule mtu aliyekuwa akizidi kuwasogelea,



"na wewe malaya sikuachi hivi hivi" Aisha aliongea huku akimgeukia Sarah kisha akaruka teke kali lililomkuta Sarah katika paji la uso na kisha kisogo cha Sarah kikagonga kwenye mti, Aisha alivyotua chini akaruka sarakasi ndogo kisha akaingia sehemu miti mingi zaidi ilipo, akakimbia huku akiwa na hasira za kushindwa kumuua Sarah wakati alimuhakikishia Harry kuwa ile kazi ingeisha usiku ule ule.



Yule bwana akafanikiwa kufika eneo lile, alikuwa ni Sajenti Minja, alifika na kumkuta msichana akiwa amefungwa pingu, Sajenti Minja akaingiza mkono mfukoni na kutoa funguo nyingi, akamfungua Sarah,



"ni nini kinaendelea?" Sajenti Minja aliuliza huku sura ya Sarah akihisi anaijua, na wakati huo Sarah nae akamtambua Sajenti Minja, mapigo ya moyo yakaongezeka,



"Mimi sijui, nilikuwa natoka hotelini naenda kutafuta usafiri, ndipo nikashangaa ananivamia na kunipiga" Sarah aliongea huku akijishika eneo la kisogoni ambapo kulikuwa na uvimbe,



"alafu wewe sura yako sio ngeni, hivi nimekuona wapi?" Sajenti Minja aliuliza,



"mhhhhhhh.....ndio tumeshawahi kuonana, kuna siku nilikuja polisi tukakutana pale nje, ulidahi umeifananisha gari yangu" Sarah aliongea huku akimuangalia Sajenti Minja,



"ooooh, nimekukumbuka. Sasa huyu aliyekushambulia unamjua?" Sajenti Minja aliuliza,



"simjui, alafu ni mwanamke" Sarah alijibu na kumfanya Sajenti Minja ashangae,



"huyo mwanamke huenda ni dada mmoja hivi hatari sana ambaye hata mimi ninamtafuta, ameshawahi kunishambulia mara mbili" Sajenti Minja aliongea huku akidhani Aisha ni Sarah na wakati huo Sarah alikuwa akimcheka Sajenti Minja chini chini.



"Mimi ni polisi, je naweza kukuchukua twende polisi ukafungue kesi?" Sajenti Minja aliuliza,



"hapana, mtu mwenyewe simjui, acha niende tu nyumbani" Sarah alijibu,



"naweza kukupeleka nyumbani?" Sajenti Minja aliuliza,



"hapana, nitaenda tu mwenyewe" Sarah alijibu,



"wewe kuwa na akili, huyo dada aliyekuvamia atakuwa bado anakuwinda, acha tu nikupeleke" Sajenti Minja alizidi kumshawishi Sarah,



"sawa nipeleke" Sarah aliitikia kisha wakatoka hapo kwenye miti na kuelekea moja kwa moja mpaka ilipo gari ya Sajenti Minja na wakaingia,



"au nikuachie uendeshe mwenyewe kwa sababu ndio unajua tuendapo" Sajenti Minja alimuuliza Sarah,http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



"hata hivyo ni sawa" Sarah aliitikia kisha Sajenti Minja akashuka na Sarah akaenda upande wa dereva, Sarah akawasha gari na kuiondoa.



"unakuja kula Vin hotel kwani huna mke?" Sarah alimuuliza Sajenti Minja,



"nani kakwambia nilikuja kula?" Sajenti Minja aliuliza huku akitabasamu,



"sasa ulienda kufanyaje?"Sarah alimuuliza,



"nilikuwa namtafuta mmiliki wa ile hotel" Sajenti Minja alijibu,



"ni ndugu yako?" Sarah alimuuliza,



"hapana, kuna maswali nataka kumuuliza" Sajenti Minja aliongea,



"ooh, nasikia ana pesa nyingi kweli" Sarah aliuliza kama kweli hamjui Taita,



"anazo, kwani wewe humjui Taita?" Sajenti Minja akamtupia swali Sarah,



"nitamjulia wapi mie" Sarah alijibu huku akiegesha gari nje ya uzio wa nyumba yake.



"nimefika, hapa ndipo naishi" Sarah aliongea,



"ni kwako au umepanga?" Sajenti Minja aliuliza,



"nimepanga" Sarah aliongea uongo huku akitabasamu,



"sasa niachie namba yako ya simu, ukihisi yule aliyekuvamia bado anakufuatilia, utanipigia" Sajenti Minja aliongea huku akiitoa simu yake, Sarah hakua na sababu ya kukataa, akampa namba Sajenti Minja.



"nilitaka kusahau, hapa unakaa peke yako au umeolewa?" Sajenti Minja aliuliza,



"nawe una maswali mengi, au kwa kuwa polisi? Mi naishi peke yangu bwana" Sarah alijibu huku akitelemka kwenye gari na pia alikuwa akitabasamu,



"kawaida kuuliza kwa mwanaume, au hupendi maswali?" Sajenti Minja aliuliza huku akiamia upande wa dereva,



"kwaheri bwana, nitakujibu siku nyingine" Sarah alijibu huku akifungua geti na kumuacha Sajenti Minja akimtupia jicho la wizi. Sarah akamuona kisha akarudi nyuma,



"nilitaka kusahau, asante kwa msaada wako" Sarah aliongea,



"usijali, ila hujaniambia jina lako" Sajenti Minja aliongea,



"naitwa Sarah" Sarah alijibu,



"haya Sarah, usiku mwema" Sajenti Minja aliaga,



"na kwako pia afisa" Sarah aliongea huku akitabasamu na kuingia ndani na kumuacha Sajenti Minja akiondoka zake.



Hiyo ndiyo ilikuwa mara ya kwanza kwa Sarah kumruhusu mtu apajue anapoishi, hakutaka iwe hivyo, ila ilitokea tu baada ya kuhisi uoga wa kufuatiliwa na Aisha, huyu mwanamke alianza kumuogopa kutokana na aina ya upambanaji wake, alikuwa anapambana kirahisi tu, ila alikuwa ni ngumu kumshinda. Sarah hakutaka kujiamini tena mbele ya Aisha kwa muda huu.



************,



Siku mpya iliwakuta Harry, Trigger na Aisha wakiwa ndani ya ofisi ya Taita wakijadiliana.



"Trigger, huyu ni Aisha nimemuongeza kwa ajili ya kazi ya kumkabili Sarah" Harry alimtambulisha Aisha kwa Trigger,



"sawa, mimi naitwa Trigger" Trigger aliongea huku akimpa mkono Aisha,



"nimefurahi kukufahamu" Aisha aliongea huku akipeana mkono na Trigger,



"sasa tujadiliane namna ya kumpata Sarah, Aisha amepata nafasi ameshindwa kuitumia" Harry aliongea,



"na wewe si nilikuambia kuna mtu alikuja na bunduki kuja kumsaidia, vinginevyo ningemuua "



"huyo aliyekuja kumuokoa ni mwenzake?" Trigger aliuliza,



"hakuna anaejua" Harry alijibu kwa ufupi,



"eti Trigger, una mbinu gani rahisi ya kumpata Sarah?" Aisha aliuliza,



"sina, aisee, labda tukambane Dokta Pendo" Trigger alijibu,



"yes, hiyo ni akili" Harry alionesha kukubaliana na Trigger, kisha wakapanga namna ya kwenda kumbana Dokta Pendo, walikubaliana kwenda usiku wa hiyo siku.



***********************



Siku hii mpya Sarah aliitumia kufuatilia masuala ya kampuni yake mpya anayotaka kuifungua na pia aliitumia kufanya manunuzi ya vitu mbalimbali vya nyumbani kwake.



Sarah aliporudi kwake nyakati za usiku, aliingia ndani ya nyumba yake na kupitia kwenye friji ambapo alichukua juisi na kwenda moja kwa moja mpaka katika chumba chake cha siri na kuingia,



"chukua juisi upoze njaa" Sarah aliongea huku akimtupia Taita box la juisi, lakini Taita hakujibu kitu wala hakuonekana kutingishika, Sarah akahisi huenda Taita anamfanyia ujanja ili amzidi akili, Sarah akatoa bastola yake,



"nyanyuka unywe juisi mbwa wewe, au nikufumue hilo litumbo lake?" Sarah aliongea kwa ukali lakini Taita hakutingishika, Sarah akamsukuma kwa mguu na kuufanya mwili wa Taita ugeuke, macho yalikuwa wazi kazi amekufa na pia damu zilikuwa zikimtoka kwenye matundu ya pua zake zote mbili, Sarah akashtuka, akaweka bastola chini na kumsogelea Taita, akapeleka mkono kifuani kuangalia mapigo ya moyo, yalikuwa kwa mbali sana, Sarah akachanganyikiwa huku asijue ni kitu gani kimemkuta Taita.



*****************



Usiku huu Dokta Pendo akiwa amevaa nguo zake za kulalia huku akiwa yupo sebuleni akitazama filamu, alisikia mlango wa sebuleni kwake ukigongwa,



"shoga amenikumbuka leo?" Dokta Pendo alijiuliza huku akihisi huyo mtu anaegonga mlango ni Sarah.



Dokta Pendo akaenda mpaka mlangoni na kufungua mlango ' yarabi toba" macho yake yalikutana hana kwa hana na mdomo wa bastola,



"habari" Aisha aliongea huku akimsogelea Dokta Pendo na kumfanya Dokta Pendo arudi nyuma bila kuongea kitu. Aisha aliingia huku akiwa ameambatana na Trigger na Harry,



"hatujaja kukuua hapa, ila ukitaka kufa tutakuua, tunataka utusaidie shida moja" Trigger aliongea huku akimuangalia Dokta Pendo lakini Dokta Pendo hakuwa na uwezo wa kujibu, alikuwa akitetemeka tu.



"mpigie Sarah na umwambie aje hapa una shida naye" Trigger alimpa maelekezo Dokta Pendo,



"namba yake sina" Dokta Pendo alijikaza na kujibu,



"nasikia ni shoga yako? Kwanini huna namba yake?" Aisha aliuliza huku akitabasamu,



"sio shoga yangu, aliniteka tu" Dokta Pendo alijijitea,



"huyu tuondoke nae, maana atatusumbua tu" Harry aliongea,



"Mimi ngoja nibakie hapa kama tulivyopanga, huenda yule mrembo anaweza kuja" Aisha aliongea,



"wewe baki, tutawasiliana" Harry aliongea huku akitoka nje ya nyumba na kumfanya Trigger amvute Dokta Pendo ili atoke,



"niache, mimi siendi popote" Dokta Pendo alilalama huku akijichomoa mikononi mwa Trigger,



"sipendagi kusumbuliwa na mabinti" Trigger aliongea kisha akamkata ngumi kali ya kichwa Dokta Pendo na kuzimia pale pale,



"khaa, wewe unampiga ngumi nzito mwanamke kama unampiga mwanaume mwenzako?" Aisha na ukatili wake wote aliogopa namna Trigger alivyomfanya Dokta Pendo,



"ukimchekea ataharibu kazi" Trigger aliongea huku akimuweka Dokta Pendo mabegani, kisha akatoka nae nje na ndani akabaki Aisha akiangaza angaza mandhari ya sebule ile.



*******************



Baada ya Sarah kuona hali ya Taita inazidi kuwa mbaya, maana hata kupumua alikuwa akipumua kwa tabu, Sarah alienda mpaka katika vifaa vyake vya matibabu na kuja na mipira ya oxygen ambayo alimuwekea Taita eneo la puani na mdomoni kisha akamtoa shati lake,



"nadhani Dokta Pendo anaweza kuwa msaada" Sarah aliongea kisha akatoka katika chumba chake cha siri na kuelekea sebuleni, akakaa koti sweta na kuelekea moja kwa moja kwenye gari, kisha akaliwasha na kuliondoa ndani ya geti kisha akaondoka kwa kasi kuelekea kwa Dokta Pendo.



Kwa jinsi alivyokuwa na haraka, gari lake hakuegesha mbali kama anavyofanyaga, leo aliiegesha pale pale mlangoni kwa Dokta Pendo.



Sarah akatelemka na kwenda kugonga mlango,



"hodi Shoga" Sarah aliita huku akigonga mlango, lakini hakujibiwa



"shoga" Sarah aliita kwa sauti kubwa zaidi huku akiendelea kugonga mlango,



"Ngoja, nakuja shoga" Sauti kutoka ndani ilimjibu, lakini haikuwa sauti ya Dokta Pendo, Sarah akapata wasiwasi, akawa anajiandaa kutoa bastola ili avamie, lakini kabla Hajaichomoa bastola yake mlango ulifunguliwa kwa kasi na Sarah akavutwa ndani, bastola ya yake ikadondoka miguuni kwa Aisha.



Sarah alipomuona Aisha alijikuta akikiasirika, haikuwa hasira ya kuvutwa au kupigwa, ilikuwa ni hasira ya kujilaumu kwanini amekuja kwa Dokta Pendo na kukutana na huyu mwanamke mbaya, Sarah hakuwa alikosa kujiamini kabisa mbele ya Aisha, uoga ukamjaa. Na wakati huo Aisha alifunga mlango kwa ndani kisha akaiokota bastola ya Sarah na kumuelekezea Sarah,



"hii ya leo haina kuremba, ni kumaliza kazi na kupotea" Aisha aliongea na kuikoki bastola huku akiwa hana tabasamu lake kama tulivyomzoea, alikuwa yupo makini kiasi kwamba ndita zilionekana vyema kwenye paji lake la uso.........



**



"kwanini utumie bunduki kuniua? Mbona unaweza kunimudu kwa mapigo" Sarah aliongea huku akimuangalia Aisha,



"kwanini tupoteze muda kwa kupigana, acha tu nimalize kazi mapema" Aisha aliongea,



"sawa, najua nakufa muda sio mrefu, je aliyekutuma uniue ni nani?" Sarah alimuuliza Aisha,



"hilo tu, nimetumwa na Harry, unamjua?" Aisha alijibu na wakati huu alianza kutabasamu,



"hapana simjui" Sarah alijibu na kukana kumjua Harry,



"siku chache nyuma nilikuona nae Vin hotel, kwanini unakataa hamjui" Aisha aliuliza,



"yule mwanasheria ndio Harry? Kakupa sababu yoyote ya yeye kutaka kuniua mimi?" Sarah alimuuliza Aisha,



"hajanipa, alafu hapa sio sehemu ya kuulizana maswali" Aisha aliongea,



"sawa, tumekutana mara mbili na Tumepambana, ulinishinda mara zote, lakini leo inaonekana kama unaniogopa na ndio maana unataka kutumia bastola" Sarah aliongea huku akimuangalia Aisha,



"nikuogope kwanini? Mimi sitaki tu kupoteza muda tena kwa ajili yako" Aisha alijibu,



"mbona umeshaupoteza tayari, maana ni muda mrefu toka tumeanza kuongea" Sarah aliongea huku akitabasamu,



"kwa hiyo unanishauri nikupige tu risasi?" Aisha aliuliza huku akiishika vyema bastola mikononi mwake,



"sawa nipige na bastola, ila hautokuwa umeshinda kihalali, ukinishinda kwa ngumi ndio utakuwa ushindi mzuri" Sarah aliendelea kumshawaishi Aisha,



"nimeshakushinda mara mbili, hiyo inaonesha tu huniwezi" Aisha aliongea kwa majivuno,



"wengi walinishinda mara mbili, ila hakuna hata mmoja aliyewahi kunishinda mara tatu" Sarah aliongea huku akitabasamu,



"sawa, mimi nitakushinda mara ya tatu, nataka niweke tofauti kati yangu na hao wengine" Aisha aliongea kisha akazimwaga risasi chini na kuitupa pembeni bastola. Sarah alikuwa na wasiwasi kwa kuwa aliutambua uwezo wa Aisha.



"twende sasa" Aisha aliongea huku akikunja ngumi tayari kupambana na Sarah.



Sarah nae akakunja ngumi kisha akaangalia namna Aisha alivyoiweka miguu yake, alimkadiria hatua.



Aisha akamuendea Sarah na kurusha ngumi nyingi za haraka, lakini hakuna hata moja iliyompata Sarah, nyingine alizikwepa na nyingine ziliishia mikononi mwa Sarah,



"umejitahidi" Aisha aliongea huku akitabasamu, kisha akaachia teke kali lililotua kwenye uso wa Sarah, Sarah akapepesuka na kwenda kujikita ukutani,



"hapo vipi?" Aisha aliuliza huku akicheka,



"Moja bila, unaongoza" Sarah alijibu huku akijifuta damu iliyokuwa ikianza kumchuruzika puani, ila kabla hata hajakaa sawa, Aisha akaachia teke jingine kama lile, Sarah akainama na lile teke likapita, Sarah akainuka na ngumi kali iliyotua kwenye pua ya Aisha, Aisha akaenda chini na damu ikaanza kumtoka puani,



"sasa hapo nimesawazisha, matokeo ni moja moja" Sarah aliongea huku akicheka ila Aisha hakutaka kujibu, sura yake ilionesha ana hasira, hakutegemea kupigwa ngumi ile.



Aisha akajinyanyua na kisha akamuendea Sarah kwa pupa, Sarah akaruka juu, Aisha akapita, Aisha alipogeuka alikutana na teke kali la mdomo lililompeleka chini tena, akatema damu,



"ubao wa matokeo unaonesha mbili kwa moja, nipo mbele" Sarah aliongea huku akijiweka sawa kwa ajili ya kuendelea na pambano, Aisha akasimama na kuhisi huenda hilo pigo alilopigwa muda huu ni makosa yake, alimuendea Sarah hovyo. Aisha akajiweka sawa, kisha akarusha ngumi kali, Sarah akainama, Aisha kwa kasi ya ajabu akampiga Sarah kifuti cha tumbo, Sarah akarudi nyuma na kujishika tumbo lake,



"mbili mbili, nimeshajua ni wapi nilikosea" Aisha aliongea kisha akarusha teke jingine, Sarah akaudaka mguu wa Aisha, kisha ule uliobakia ardhini aliupiga teke kali na Aisha akadondoka chini kama mzigo,



"tatu hiyo" Sarah aliongea huku akiwa ameinamisha kichwa, Aisha akanyanyuka kwa mtindo wa ajabu na kuachia ngumi, Sarah akaiona akaachia teke lilikutana na ile ngumi, Aisha akapuliza mkono kutokana na maumivu aliyoyapata, Sarah akaruka juu na kutua kwenye kifua cha Aisha na teke kali, Aisha akaanguka chini, Sarah akamsogelea na kumpa mkono kwa lengo la kumpa msaada ili Aisha asimame, Aisha akaushika mkono wa Sarah kisha akamvuta ili Sarah aanguke chini, Sarah aliliona hilo, alichofanya ni kuupeleka mguu wake ukutani kisha akamvuta Aisha kwa nguvu na Aisha akakutana na kichwa cha pua, Aisha akahisi kizunguzungu, Sarah akamuachia na kisha akamrushia ngumi kali iliyoenda kwenye paji la uso wa Aisha, Aisha pumzi ikakata, akaanguka chini na kupoteza fahamu.



"aaaaagh hii haikutakiwa, kilichotakiwa ni kuendelea kupambana mpaka asubuhi" Sarah aliongea huku akilaani kitendo cha Aisha cha kupoteza fahamu.



Sarah Akaingia chumbani kwa Dokta Pendo na kuangalia kama yupo lakini hakubahatika kumuona, akarudi sebuleni na kufanya kuokota bastola yake, akazirudishia risasi na kutoka zake nje, akaingia ndani ya gari lake na kuliondoa huku akiwa amekata tamaa ya kupata msaada kutoka kwa Dokta Pendo.



Sarah aliendesha gari yake mpaka nyumbani kwake na kuiingiza ndani ya geti, kisha akatelemka haraka haraka na kukimbilia ndani, alielekea moja kwa moja mpaka katika chumba chake cha siri, akafungua mlango na kuwasha taa, akakuta bado Taita amelala hajitambui, Sarah akamtoa machine zilizokuwa puani ambazo zilikuwa zikimsaidia Taita kupumua, kisha akajaribu kumbeba, akashindwa, akataka kumvuta mkono ili ampeleke nje, akashindwa, Sarah akasimama huku akionesha kuna jambo analifikiria, baada ya dakika moja alitoka kwenye kile chumba na kurudi na kiti cha matairi, akakisogeza jirani na kitanda alicholala Taita, kisha akamsukuma Taita na kuangukia kwenye kile kiti cha matairi, kisha Sarah akashusha pumzi ndefu na kukiendea kile kiti, kisha akaanza kukisukuma kuelekea nje, alikisukuma kile kiti cha magurudumu mpaka nje ya nyumba ila ndani ya uzio, akamuweka Taita chini, akamlaza kwenye marumaru. Aliamua kumtoa Taita nje ili apate hewa ya kutosha kwa maana pale nje ni eneo la wazi,



"mbona unataka kufa mapema hivi, tena kifo kirahisi kisicho hata na majeraha?" Sarah aliuliza huku akimuangalia Taita ambaye hakuwa na fahamu,



"ebu subiri" Sarah aliongea huku akielekea getini na kuhakikisha kama amelifunga vizuri, kisha akarudi mpaka kwenye chumba chake cha siri na kuchukua panga kubwa na mkuki, kisha akatoka navyo mpaka alipokuwa amelala Taita,



"si bora nikutoboe macho kisha mwili wako niukate kate vipande, huenda kifo chako kitakuwa cha maumivu" Sarah aliongea huku akiwa amesimama pembeni ya mwili wa Taita na mkononi alikuwa na panga,



"aaaaagh, bora nikakutupe tu, ufe ingawa kifo chako sijakipenda" Sarah aliongea na kutupa lile panga kwa hasira, kisha akaelekea kwenye gari lake na kuingia, akaliwasha na kulisogeza mpaka jirani na mwili wa Taita, kisha akafungua mlango wa nyuma wa gari na kujitahidi kumnyanyua Taita na kumtupia ndani ya gari, kisha na yeye akaingia kwenye gari yake na kuitoa nje ya geti, kisha akatelemka kwenye gari na kurudi kufunga geti, kisha akarudi kwenye gari na kuliondoa.



*******************



Nyakati hizi za usiku, Sajenti Minja alikuwa njiani kuelekea nyumbani kwake, alikuwa ndani ya gari, alipofika maeneo ya mataa ilibidi asimamishe gari kutokana na taa nyekundu zilizopo mbele yake, Sajenti Minja akaisimamisha gari yake na kuangalia magari mengine yaliyoruhusiwa kupita, sasa hapo ndipo akashtuka, aliiona ile Range Rover nyeusi ikikatiza mbele yake, Sajenti Minja akaitupia jicho ile gari.



Taa za barabarani ziliporuhusu upande alipo Sajenti Minja, Sajenti Minja alishika uelekeo ilipoelekea ile Range Rover nyeusi, kwa bahati nzuri aliiona baada ya mwendo mfupi, akaanza kuifuatilia, mara ya kwanza alidhani ile gari ni ya Sarah, ila aligundua namba za ile gari ni zile namba za ile gari ya mwanzo ambayo mmiliki wake alipambana nae kwenye nyumba iliyoungua, kitu ambacho Sajenti Minja hakukijua ni kuwa huyo Sarah na huyo binti waliyepambana naye mwanzo ni mtu yule yule ambaye ni Sarah.



Sajenti Minja akaongeza mwendo wa gari ili aweze kumdhibiti Sarah.



Sarah wakati akiwa anaendesha gari yake, aliweza kugundua kuna gari inamfuatilia, alichofanya ni kuongeza mwendo wa gari yake, aliamini kuwa gari yake ni moja kati ya magari machache yenye kasi, na kwa hilo Sarah alikuwa sahihi, aliweza kuendesha na kuiacha mbali sana gari ya Sajenti Minja, kisha akabadili uelekeo ili kumpoteza kabisa huyo anayemfuatilia, mara ya kwanza alikuwa anaenda beach kumtupa Taita, ila sasa aliamua kwenda dampo, kuna jalala kubwa alilifahamu ambalo lipo kwenye eneo lililojificha na pia lilikuwa likitisha kutokana na vibaka wengi kuishi eneo hilo.



Sarah alivyofika eneo hilo, alishuka kwenye gari na kuanza kukagua mazingira yale kama kuna mtu yoyote anaweza kuwepo kwenye mazingira yale, alijiridhisha hakuna mtu na pia akiwa amejiaminisha kuwa hata yule aliyekuwa akimfuatilia hawezi tena kufika hapo, Sarah alienda kwenye mlango wa nyuma wa gari yake na kuufungua, akamtoa Taita, kwa kuwa hakuwa na nguvu ya kumbeba, alichofanya ni kumbingirisha tu, alimsukuma mpaka kwenye mtelemko uliopo mwishoni mwa dampo, kisha akauachia hapo mwili wa Taita ukiwa unaseleleka kuelekea bondeni, Sarah akawa amechuchumaa akiuangalia namna unavyobingirita,



"dah, sijapenda, amekufa kirahisi sana" Sarah aliongea peke yake kisha akisimama, alipogeuka nyuma akakuta mtu akiwa amesimama kama hatua kumi kutoka alipo yeye na alikuwa akimuangalia, ila kutokana na giza lile ilikuwa ngumu kuonana sura, Sarah akajipapasa kiunononi kuiangalia bastola yake, hakuikuta, akakumbuka ameisahau ndani ya gari, wakati Sarah akiendelea kutafakari huku akijiuliza yule mtu ni nani usiku ule, pembeni ya yule mtu akaongezeka mtu mwingine, Sarah akachoka kabisa, na muda huo wale watu wawili wanaume wakaanza kupiga hatua kuelekea alipo Sarah, Sarah alipotazama nyuma kuangalia njia nyingine, bahati mbaya hakukuta njia, njia ilikuwa moja tu, ambayo ndiyo hiyo iliyo mbele yake na ubaya kuna wanaume wawili walikuwepo wanamfuata.............





Sarah akaanza kurudi nyuma huku hofu ikimzidi,



"sister saula, hili chaka uliloingia sio" kijana mmoja aliongea kwa sauti nyembamba iliyotokea puani na kumfanya Sarah ajue kuwa huyo ni teja,



"fasta kabla hatujakugeuza bucha" kijana wa pili aliongea huku akivuta panga kutoka kiunoni mwake.



"ngojeni, mnataka nini?" Sarah aliuliza huku akirudi nyuma,



"toa kila kitu sister" kijana wa kwanza alijibu huku akiwa karibu kabisa na Sarah, Sarah akapiga hesabu za haraka haraka kisha kwa kasi ya ajabu akamruka kijana wa kwanza na kutua mbele ya kijana wa pili yule mwenye panga, yule kijana akabaki na mshangao kwa namna Sarah alivyofanya,



"habari yako" Sarah aliongea huku akimuangalia yule kijana kisha Sarah akaachia teke kali lililomkuta yule kijana usawa wa shavu, yule teja akaenda chini na panga likamtoka mkononi, kisha Sarah akapiga sarakasi ndogo na kuokota lile panga kisha akageuka nalo na kumkuta yule kijana mwingine akija kwa kasi huku akiwa na bisibisi mkononi, Sarah akapiga hatua moja kumuelekea kisha akamuwekea panga shingoni kama anataka kumchinja,



"shida nini baba?" Sarah alimuuliza huku akitabasamu, lakini yule kijana hakujibu kitu, alikuwa akitetemeka tu, Sarah akatoa panga shingoni kwa yule kijana kisha akalitupa panga chini na kuondoka zake kwa mwendo wa haraka na kuwaacha wale vijana wakimuangalia tu huku wasiamini kile walichofanyiwa.



Sarah akaelekea kwenye gari lake na kuingia kisha akaliondoa kwa fujo kurudi nyumbani kwake huku akifungua mziki mzito ndani ya gari.



Sarah alifika nyumbani kwake na kukimbilia kwenye kioo na kujiangalia usoni kama amedhurika na mapigo ya Aisha, hakuona jeraha lolote,



"mpumbavu yule, amekariri pigo la aina moja tu, siku nyingine namuua ili huyo Harry apate fundisho" Sarah aliongea huku akielekea kwenye chumba chake cha siri na kukisafisha kisha akaelekea bafuni kuoga huku akiisubiri siku mpya ambayo aliamini itakuja na habari mbaya kumuhusu Taita.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



**************.



Aisha alishtuka asubuhi akiwa amelala sakafuni huku akiwa na maumivu na damu baadhi ya sehemu za mwili,. Aisha akajivuta na kusimama, alijitahidi kuinuka ingawa alihisi mwili ukimuuma, akaenda kukaa kwenye kochi na hapo ndipo kumbukumbu zikamrejea juu ya tukio lililomkuta mpaka akafikia katika hali aliyokuwa nayo muda huo,



"kumbe yule mwanamke ni mwendawazimu" Aisha aliongea baada ya kukumbuka alichofanyiwa na Sarah, na hapo akahisi mlango ukigongwa, Aisha akanyanyuka na akauendea mlango kwa tahadhari sana huku mkononi akiwa na bastola yake, nae mgongaji hakuchoka kugonga mlango, aliendelea tu, na safari hii alizidisha nguvu ya ugongaji.



Aisha akausogelea mlango kisha akaangalia na kugundua upo wazi, akapiga hatua tatu nyuma na kuishika vizuri bastola yake, aliielekezea mlangoni,



"karibu, mlango upo wazi" Aisha aliongea huku macho yakiwa mlangoni, mlango ukafunguliwa na kisha mgongaji akaingia ndani,



"wewe ni mimi, usipige risasi" Harry aliongea baada kuingia ndani na kukutana na mdomo wa bastola,



"kumbe ni wewe boss, nilijua yule malaya amerudi tena" Aisha aliongea huku akikaa kwenye kochi, Harry akamtazama sura yake na kuona jinsi ilivyokuwa nyekundu, Harry hakupata tabu kugundua kuwa sura ya Aisha kuwa vile ni kutokana na kipigo,



"nani, Sarah?" Harry aliuliza,



"ndio huyo huyo" Aisha alijibu huku akiangalia pembeni,



"alikuja muda gani?" Harry aliuliza,



"muda mchache baada ya nyinyi kuondoka" Aisha alijibu,



"hujamuua?" Harry aliuliza swali la kizembe,



"wewe mjinga nini, ningekuwa nimemuua ungenikuta nimeshika bastola namna ile?" Aisha aliuliza kwa jazba baada ya kuhisi Harry anamdhiaki,



"ilikuaje sasa?" Harry aliuliza,



"ameingia hapa na nimemdhibiti vizuri tu, ila nimefanya kosa dogo ndio amefanikiwa kunikimbia" Aisha aliongea,



"umemdhibiti au alikudhibiti? kama wewe uliyemdhibiti upo kwenye hali hiyo, je huyo aliyedhibitiwa yupoje?" Harry aliuliza,



"naona imani imepungua kwangu, ni bora niachane tu na kazi yako kama huniamini" Aisha aliongea,



"nakuamini sana Aisha, ila naona kama kazi imekuwa ngumu kwako ila unashindwa kukubaliana na hilo jambo" Harry aliongea,



"mzee unatakiwa utulie, kazi naifanya mimi, nikishindwa nitakurudishia pesa yako uliyonipa hawali" Aisha aliongea kwa jeuri,



"basi yaishe, tunatakiwa kuondoka muda huu, maana hapa sio kwetu" Harry aliongea huku akinyanyuka kwenye kochi na Aisha nae akasimama kisha wakatoka zao ndani ya ile nyumba ya Dokta Pendo na wakaondoka zao.



**** *********



Dokta Pendo alikuwa bado amefungiwa kwenye chumba kidogo ambacho hakikuwa na hewa ya kutosha, na isitoshe alikuwa amepigwa sana kutokana na kiburi chake cha kutosema ukweli kuhusu njia ya kumshika Sarah, Dokta Pendo alikuwa Hoi bin taaban, hawezi kutembea, miguu ilikuwa imevunjwa na Trigger, Dokta Pendo alibakiwa na sauti ya kuongelea,



"ujue mimi nitakuua, sifanyi utani, nipe namba za Sarah" Trigger aliongea huku akiwa amevaa vest iliyokuwa na damu sehemu kubwa,



"niue tu, maana hicho ndicho kilichobakia, niue, unasubiri nini!?" Dokta Pendo aliongea kwa uchungu huku akilia, Trigger akamrushia konde zito na kumpiga Dokta Pendo ngumi ya mdomo, Dokta Pendo akapiga kelele za maumivu,



"kuua ni jambo dogo tu kwangu, tena kwa mtu jeuri kama wewe uwa nafurahi sana ninapokuua" Trigger aliongea huku akitoa tabasamu la kifedhuli bila kujali maumivu anayoyapata Dokta Pendo,



"najua wewe ni muuaji mzuri, na ndio maana mkamuulia Sarah wazazi wake na pia mkamteka babu yake" Dokta Pendo aliongea kwa hasira, alishaamua liwalo na liwe,



"kumbe mnakaaga na kuongea hayo mambo eeh?" Trigger aliuliza huku akiokota kipande cha nondo, alipania kumpiga nacho Dokta Pendo kichwani,



"Niue, nimalize nikapumzike" Dokta Pendo aliongea huku akikilaza kichwa chake sakafuni, alishajikatia tamaa. Trigger akakinyua juu kile kipande cha nondo, Trigger alidhamiria kummaliza Dokta Pendo, Trigger aliinyanyua nondo juu, kisha akawa anajiandaa kuishusha kichwani kwa Dokta Pendo,



"wewe vipi? Usimpige bwana" Harry aliongea huku akiingia mule ndani, aliongozana na Aisha,



"ana kiburi sana, ananijibu hovyo" Trigger aliongea huku nondo ikiwa bado ipo hewani,



"sasa ukimuua si ndio utaharibu kabisa, utakuwa umeharibu mtego wetu" Aisha aliongea huku akimtazama Trigger,



"Trigger hizo bangi unazotumia kwa sasa hazikupeleki vizuri, unakuwaje sijui, yaani hujielewi kabisa" Harry alimlaumu Trigger,



"kumuacha huyu itakuwa kosa kubwa sana" Trigger aliongea huku akiwa bado anaonesha hasira za wazi kwa Dokta Pendo,



"Aisha ebu mchukue huyo dada na umpeleke kule chumba kingine" Harry aliongea kisha Aisha akaenda sehemu alipo Dokta Pendo na kumnyanyua, cha ajabu Dokta Pendo alishindwa kusimama, alikuwa akilia tu,



"Boss, huyu miguu hana tena, tayari imeshavunjwa" Aisha aliongea huku akimtazama Harry,



"dah, Trigger bangi unazovuta sasa hivi zinakukataa, unakuwa kama kichaa, yaani hueleweki kabisa" Harry alimlaumu Trigger ambaye alikuwa akivaa fulana yake,



"huyu sio wa kuwekwa ndani, tuangalie namna ya kumfikisha hospitali" Aisha aliongea kwa huruma,



"huyu tukimpeleka hospitali itakuja kuwa shida kwetu akipona" Trigger aliongea kwa hasira,



"Aisha ebu toka nje mara moja" Harry aliongea huku anamuangalia Aisha, Aisha akaenda zake nje, ingawa alihisi kuna jambo baya linaweza kutokea juu ya Dokta Pendo. Aisha akaenda zake nje,



"wewe unataka tufanye nini? " Harry alimuuliza Trigger,



"huyu afe tu, hakuna njia nyingine" Trigger alijibu,



"usimuue, maana hapo alipo tayari hana uwezo wa kuishi hata siku mbili, cha msingi ni kwenda kumtupa tu" Harry alitoa ushauri,



"sawa, hilo nalo ni wazo zuri" Trigger aliongea,



"sawa, usiku utafanya hivyo" Harry alimwambia Trigger,



"poa" Trigger aliongea kisha wakawa wamemaliza kwa mtindo huo, wakaachana na kila mmoja akaelekea kwenye jukumu lake.



*******************



Asubuhi hii ilimkuta Sajenti Minja akiwa ofisini kwake na mawazo yalikuwa juu ya ile gari nyeusi ambayo inamilikiwa na mwanamke ambaye alimchukulia ni hatari sana, na mbaya zaidi usiku uliopita aliweza kuiona hiyo gari na alijaribu kuifukuzia lakini hakuipata.



Akiwa kwenye mawazo hayo, alishtuliwa na simu yake iliyokuwa inaita, alipotupia macho kwenye kioo cha simu, alikuta jina la bosi wake, akapokea simu haraka,



"naam mkuu" Sajenti Minja aliongea kikakamavu,



"nenda eneo la dampo kuu, kuna mwili wa mtu umeokotwa" Mkuu wa polisi aliongea na kukata simu.



Sajenti Minja akainuka na kutoka mpaka kwenye gari yake, akaingia na safari ya kwenda dampo kuu ikaanza, ilimchukua dakika kumi kufika dampo kuu.



Alishuka na alikuta kuna askari wengine wakiwa eneo hilo, na ndani ya gari walikuwa wameupakia mwili. Sajenti Minja akawasalimu wenzake, kisha akatupia macho kwenye ule mwili, ndipo alipomuona mtu mzima akiwa amelala, alikuwa ni Taita, ila Sajenti Minja hakuweza kumjua kwa kuwa mwili wa Taita ulikuwa umevimba.



"mmepata habari yoyote kuhusu huu mwili?" Sajenti Minja aliuliza,



"kuna vijana wawili wanadai walimuona mtu aliyekuja kuutupa mwili" askari mmoja alijibu,



"wako wapi?" Sajenti Minja aliuliza,



"wale pale waliokaa pale" askari aliongea huku akiwaoneshea kidole,



"kwanini mmewaacha sasa?" Sajenti Minja aliuliza kwa ukali,



"tumewaona ni mateja, tukahisi wanataka pesa tu" askari alijibu,



"wajinga kabisa nyie, huo ndio ushahidi, niwakute ofisini kwangu wale vijana" Sajenti Minja aliongea huku akielekea mahali ilipo gari yake, kisha akaiwasha na kuondoka.



***************/****



Sajenti Minja alirudi ofisini kwake na kuwakuta wale vijana wakiwa nje ya ofisi yake wakimsubiri, Sajenti Minja akawasalimia kisha akawataka waingie ofisini,



"bila kupoteza muda, mnaweza kunieleza chochote kuhusu ule mwili uliookotwa kule dampo kuu?" Sajenti Minja aliuliza huku akiwatupia jicho,



"sisi tuliona gari nyeusi kali, ikipaki, kisha tukamuona mwanamke akishuka na kwenda kufungua mlango wa nyuma wa gari na kumtoa mtu na kwenda kumtupa" Teja wa kwanza alielezea, kipindi chote Sajenti Minja alikuwa amesisimka mwili kutokana na maelezo ya huyo Teja, kwani mtu anayezungumziwa ndiye yule yule anayemtafuta.



"huyo mwanamke mlifanikiwa kumuona kwa karibu?" Sajenti Minja aliuliza,



"tulimuona vizuri ingawa kulikuwa na giza, Maana tulimfuata" Teja wa kwanza alijibu,



"Mimi mpaka gari yake naijua, nimeikariri vizuri tu" Teja wa pili aliongezea,



"namba za gari yake umezikariri?" Sajenti Minja aliuliza,



"sio namba, ile gari nimeikariri tu, range Rover nyeusi" Teja wa pili alijibu,



"majina yenu" Sajenti Minja aliuliza huku akiwaangalia,



"mi naitwa Juma John" Teja wa pili alijibu na Sajenti Minja akaandika,



"andika salum dengo" Teja wa kwanza akajibu na kisha Sajenti Minja akaandika,



"mnaweza kwenda, ila mkimuona huyo dada au mkiiona gari yake, mje mnipe taharifa, nitawapa pesa" Sajenti Minja aliongea,



"usijali kamanda, tutakutimbia tukimdekshia" Teja wa kwanza aliongea huku wakitoka nje na kumuacha Sajenti Minja akiwaangalia huku akitabasamu.



Wale mateja wakatoka mpaka nje ya ofisi, na wakati huo Sarah alikuwa akiegesha gari yake nje ya ofisi za polisi. Wale mateja wakamuona,



"mzeebaba, yule dada si yule pale" Teja wa kwanza aliongea huku akimtazama Sarah aliyekuwa akatelemka kwenye gari,



"ndio yeye, hata gari ndio lile lile" Teja wa pili alijibu,



"wewe baki hapa mtazame anapoelekea, mimi ngoja nikamtonye kamanda" Teja wa kwanza aliongea huku akielekea ofisini kwa Sajenti Minja. Alipofika aliingia moja kwa moja ofisini, mpaka Sajenti Minja akashtuka,



"Baba kama zali, huyo demu Aliyefanya unyambilisi nae ndio anaingia kituoni, yupo hapo nje" Teja alitoa taharifa iliyomsisimua Sajenti Minja,



"yupo nje?" Sajenti Minja aliuliza kama hakusikia vile,



"Babu tuwahi, tusipoteze muda" Teja aliongea huku akigongesha mikono kwa msisitizo.



Sajenti Minja akanyanyuka na kuanza kuelekea nje, huku yule teja akija kwa nyuma yake na mwendo wake wa kutembea bega moja likiwa chini.........





Wakati Sajenti Minja na yule kijana Teja wakiwa ndani wanaelekea nje, ndio muda ambao Sarah alikuwa analiondoa gari lake eneo la polisi, aliamua kuliondoa gari baada ya kuwaona wale vijana mateja wakiwa wanajadiliana, na alipowaangalia vizuri aliwagundua kuwa wale vijana ndio alikabiliana nao usiku uliopita wakati alipoenda kumtupa Taita kwenye dampo kuu.



Sarah aliondoka kwa ajili ya usalama wake, na hapo polisi alienda kwa ajili ya kuitikia uito alioitwa baada ya kutakiwa kuja kukamilisha masuala ya kampuni yake hasa upande wa usalama.



Huku nako Sajenti Minja na yule kijana Teja walikuwa ndio wanafika nje, ila hawakuikuta gari ya Sarah,



"wewe yule duu yukwapi?" Teja aliyetoka ndani alimuuliza mwenzie aliyemuacha nje,



"amesepa, alivyoshuka kwenye gari, nikamuona amerudi tena ndani ya gari na kuondoka" Teja aliyekuwa nje alimjibu mwenzie na kufanya Sajenti Minja acheke tu,



"ila usijali mzeebaba, atakuja tena, msubiri hapa hapa nje" Teja aliyetoka ndani aliongea huku akimpiga piga begani Sajenti Minja,



"sema yule dada ana sura nzuri ila haendani na matendo yake, amechafukwa roho" Teja aliyekuwa nje aliongea huku akicheka peke yake,



"mi acha nirudi ofisini, nyie endeleeni kumtafuta tu" Sajenti Minja aliongea huku akiondoka na kuwaacha mateja hapo nje.



"poti mbahili kweli, yaani juhudi zote tunazoonesha lakini ameshindwa kututoa hata buku mbili?" Teja aliyekuwa nje alimuuliza mwenzake huku wakipiga hatua za kuondoka eneo hilo,



"mchaga huyo, kwanza anaitwa Minja, nimeona ofisini kwake juu ya meza kuna kibao kimeandikwa SJT MINJA, sasa sijui maana ya hiyo SJT ni nini?" Teja aliyetoka ndani aliuliza,



"litakuwa ndio jina lake" Teja aliyekuwa nje alijibu huku wakipotea katika eneo lile la kituo kikuu cha polisi.



****************



Harry baada ya kukubaliana na Trigger kuwa Dokta Pendo anatakiwa kutupwa Nyakati za usiku, Harry alimkabidhi hiyo kazi Aisha, yaani kazi ya kumtupa Dokta Pendo aifanye Aisha,.



Kisha Harry akaingia ndani ya gari yake ili aelekee ofisini, alipoingia ndani ya gari simu yake ikaanza kuita, alipoangalia namba ya mpigaji ikambidi apokee,



"nakuja, nipo njiani" Harry aliongea baada ya kupokea simu,



"unakuja wapi?" Sauti iliuliza upande wa pili wa simu,



"ofisini" Harry alijibu huku akionekana kupenda maswali hayo aliyokuwa akiulizwa na secretary wake,



"Mimi nipo hospitali, boss Taita ameokotwa hakiwa hajitambui" upande wa pili wa simu ulitoa habari iliyonifanya Harry achanganyikiwe, hakuamini kusikia habari hiyo,



"hospitali gani?" Harry aliuliza,



"MTC hospitali, wodi namba 21" upande wa pili wa simu ulijibu,



"kwa watu mahututi?" Harry aliuliza,



"nilipokwambia yupo mahututi hukunielewa?" upande wa pili wa simu uliuliza huku ukionekana haukufurahia swali la Harry,



"ok, nakuja" Harry aliongea na kukata simu, hakuonekana kuzifurahia hizo habari, maana Harry alishaamua kuwa huru na kuachana kabisa na mambo ya kiharifu, ila kilichokuwa kinamtisha ni Taita tu, maana alishasema mtu yoyote atakayejitoa kwenye vita dhidi ya Sarah atakuwa ni msaliti, na adhabu yake ni kifo.



Harry alikuwa hana furaha, furaha ingekuwepo endapo angesikia Taita amekufa,



"aisee, kwanini hujafa Dennis?" Harry aliongea huku akiuma meno yake kwa hasira, kisha akashika njia inayoekea MDC hospitali huku akimlaumu Sarah kwa kumuacha Taita akiwa hai,



"yaani angekufa Taita, kazi yangu ingekuwa ni kummaliza Sarah pekee" Harry aliongea huku akiongeza mwendo wa gari yake.



Baada ya nusu saa gari ya Harry ilikuwa ikipaki nje ya MDC Hospitali, akashuka na kuelekea moja kwa moja sehemu ilipo wodi namba ishirini na moja na kwa bahati nzuri aliweza kumuona Taita kupitia kioo cha mlangoni, hakuna mtu aliyeruhusiwa kuingia ilipokuwa madaktari tu.



"vipi hali ya mgonjwa?" Harry alimuuliza secretary wake aliyemkuta pale,



"sio nzuri kwa kweli, ni kumuomba Mungu tu" Secretary alijibu,



"wamegundua tatizo?" Harry aliuliza,



"bado, hapo walichofanya ni kumtundikia dripu za damu tu mpaka fahamu zitakapomrejea ndio wamfanyie vipimo vingine" secretary aliongea,



"dah, polisi hawajaja?" Harry aliuliza,



"toka nimekuja sijawaona, ila naskia waliomleta ni polisi" secretary alijibu,



"sawa, wewe rudi kazini kuendelea na kazi, acha mimi niwe huku leo" Harry alimwambia secretary wake,



"sawa, kwa hiyo watu wakija kukuulizia kazini niwaambiaje?" secretary aliuliza,



"waambie ukweli tu" Harry aliongea,



"sawa, naenda" secretary aliaga lakini Harry hakujibu, badala yake aliingiza mkono mfukoni na kutoa simu yake, akatafuta namba anayoitaka na kupiga, kisha akapiga, simu ikaita muda na kupokelewa,



"hallow Vin, vipi?" Harry aliongea,



"safi, za uko?" Vin alijibu kwa sauti ya uchovu,



"vipi mbona unaongea kwa unyonge hivyo?" Harry aliuliza,



"nilikuwa nimelala, si unajua tunapishana masaa?" Vin aliongea,



"kweli, hivi mara ya mwisho kuongea na baba yako ni lini?" Harry alimuuliza Vin,



"nilimpigia siku za karibuni lakini hakuwa anapatikana, vipi kwani?" Vin aliuliza,



"oooh, basi kuna tatizo limetokea kidogo, mzee amepata tatizo" Harry aliongea,



"tatizo gani tena?" Vin aliuliza utasema hakuwa ametoka Kulala muda mchache uliopita,



"mzee alipotea siku chache hizi na hakuna aliyejua ni wapi alipo, ila mwili wake umeokotwa leo asubuhi akiwa hajitambui" Harry alitoa taharifa iliyomchanganya kabisa Vin, maana alimpenda sana baba yake,



"mbona hukunipa taharifa mapema?" Vin aliuliza huku akiwa na hasira,



"ujue Vin mzee wako ni kawaida kupotea mjini hata mwezi mzima, kwa hyo kupotea kwake siku hizi chache tuliona ni jambo la kawaida tu na ndio maana hatukukupa taharifa" Harry alijitetea,



"madaktari wanasemaje?" Vin aliuliza,



"madaktari wanasema ni kweli mzee yupo kwenye hali mbaya, wanadai watapambana kujaribu kumrejesha katika hali yake" Harry alijibu,







"nakuja, itakuja nije wiki hii" Vin aliongea,



"sawa boss" Harry alijibu na kukata simu.



Simu ilipokatwa, Vin akanyanyuka kitandani na kuelekea sebuleni kwake, akachukua simu na kupiga uwanja wa ndege ili kuulizia kama anaweza kupata ndege ya kwenda Africa mashariki, kwa bahati nzuri aliweza kupata ndege inayoelekea Kenya, akaomba awekewe nafasi na kuwapa ahadi ya kwenda kulipia hiyo tiketi siku inayofuata, asubuhi.



Vin akakata simu huku akiwa anaonekana hana raha kabisa, kwa maana aliamini mtu muhimu aliyebaki duniani ni baba yake huyo tu, Vin alikuwa amechanganyikiwa ndani ya muda mfupi, akili yake ilifanya kazi haraka mno kipindi anapokuwa na tatizo, na hata kitendo cha kupiga simu uwanja wa ndege ni matokeo ya akili yake kufanya kazi haraka,



"Mungu nilindie baba yangu, akiondoka huyo mimi sitokuwa mtu tena, hakuna mtu mwngine anayenipenda kama yeye" Vin alisali huku akiwa amepiga magoti chini, kitu ambacho hakukijua ni kuwa mtu anayedhani ni mwema kwake na anayedhani ni baba yake, ndiyo huyo mtu aliyeiangamiza familia yake.



*****, **************



Asubuhi iliyofuata, Sarah aliamka huku akiwa amepanga kupumzika tu siku hiyo, ila akakumbuka kuna mtu ambaye tayari amemsababishia matatizo, na Sarah kamwe hakutaka kumuingiza mtu matatizoni, alishaamua hii kazi ya kulipa kisasi ni ya kwake, ila kilichokuwa kinamnyima raha muda huo ni kutekwa kwa Dokta Pendo,



"ebu ngoja niende kwake, labda wamemuachia" Sarah aliongea huku akinyanyuka na kuelekea nje kwenye gari lake ili akamuangalie Dokta Pendo.



Aliingia kwenye gari na kuondoka zake mpaka kwa Dokta Pendo, alishukia mbali na kusogea kwa miguu mpaka mlangoni kwa Dokta Pendo, akakuta nyumba imepigwa kufuri kumaanisha hakuna mtu.



Sarah akarudi kwenye gari na kuelekea zake kazini kwa Dokta Pendo, kule hospitali, ilimchukua dakika kumi Sarah kufika kazini kwa Dokta Pendo, akaegesha gari na kutelemka, akaelekea moja kwa moja mpaka mapokezi na kumsalimia dada wa mapokezi,



"Dada samahani, Dokta Pendo nimemkuta?" Sarah aliuliza ili kujua Kama Dokta Pendo yupo uraiani au bado ametekwa?



"ulikuwa na mihadi nae?" Dada wa mapokezi aliuliza,



"ndio, ni mgonjwa wake pia ni rafiki yake" Sarah aliongea,



"kuna habari mbaya, Dokta Pendo ameokotwa leo asubuhi hii akiwa hajitambui na miguu yake yote ilikuwa imevunjika" Dada wa mapokezi aliongea na kumfanya Sarah mwili umsisimke,



"yupo wodi namba ngapi?" Sarah aliuliza huku machozi yakimtoka, aliamini endapo Dokta Pendo atakufa, basi hilo ni kosa lake yeye Sarah,



"hayupo hapa, polisi walimuokota na kumpeleka MDC Hospitali, yupo uko wodi namba ishirini na mbili" Dada wa mapokezi alijibu,



"sawa, acha nikamuone" Sarah aliongea huku akiondoka na sura yake iligubikwa na majonzi makubwa kutokana na habari alizopewa na Dada wa mapokezi.



Sarah alipanda kwenye gari lake na kuliondoa kuwahi hospitali.



Alifanikiwa kufika MDC hospitali na kuingia moja kwa moja kwenye wodi aliyolazwa Dokta Pendo ambayo ipo jirani kabisa na wodi aliyolazwa Taita.



Sarah alienda mpaka kwenye mlango wa wodi na kutaka kufungua,



"samahani dada, huruhusiwi kuingia ndani, muangalie kupitia vioo vya hapo hapo mlangoni" Muuguzi mtu mzima aliongea huku akimzuia Sarah kuingia ndani,



"oooh samahani, sikujua" Sarah aliongea,



"nakuona una majonzi sana, mgonjwa ni nani yako?" Muuguzi alimuuliza Sarah,



"ni rafiki yangu" Sarah alijibu,



"pole sana" Muuguzi alimwambia Sarah,



"asante" Sarah aliongea huku akifuta machozi,



"nenda kapumzike mwanangu, urudi baadae" Muuguzi aliongea huku akimpiga piga begani Sarah aliyekuwa analia.



Sarah baada ya kubembelezwa, aliamua kuondoka eneo la hospitali, wakati Sarah akiondoka na muda huo ndio Sajenti Minja na wale vijana mateja ndio walikuwa wakiingia hospitali, wakapishana huku Sarah akiwa ameweka mkono machoni akifuta machozi, huku uso wake akiwa ameuinamisha chini, wao Sajenti Minja na wale vijana mateja walikuwa macho mbele bila kutazama mtu wanaepishana nae. Yaani kiufupi hakuna aliyemuona mwenzake.



Baada ya kupishana Teja mmoja akatupa jicho nyuma, na wakati huo Sarah alikuwa a akirudisha kitambaa kwenye mfuko wa nyuma wa suruali, wakati anatoa mkono mfukoni, Sarah mkono wake ukatoka na pesa ikadondoka, ila Sarah hakuona isipokuwa kuwa Teja,



"Dada ameangusha pesa" Teja aliongea na kufanya wenzake wageuke nyuma,



"leo umekua mstaharabu, kaiokote ituokoe" Teja mwenzake aliongea,



"kaiokote umrudishie, mkitembea na mimi mnatakiwa kuwa wastaharabu" Sajenti Minja aliongea huku akisimama na kumtupia jicho yule dada ambaye alikuwa amewapa mgongo na anazidi kwenda.



Teja yule aliyeona wakati Sarah akiangusha pesa, aliiendea ile pesa na kuiokota kisha akamkimbilia Sarah, alipofika akamshika bega,



"Dada umeangusha hela" Teja aliongea na Sarah akasimama, akawa anajiandaa kugeuka huku yule kijana Teja akimsubiri na pia Sajenti Minja na yule kijana Teja mwingine walikuwa wakiangalia





Sarah alisimama ila alisita kugeuka, hiyo sauti iliyomsimamisha aliijua vizuri, Sarah akaamua asonge mbele bila kugeuka nyuma, hata kuongea hakutaka, akamuacha yule kijana Teja akimshangaa tu. Sarah akapotea machoni kwake, yule kijana Teja akageuka na kukuta wenzake wakitabasamu,



"hiyo bahati yako, iweke mfukoni" Sajenti Minja aliongea huku akitabasamu,



"kweli ridhiki mafungu saba" Teja aliongea huku akiiweka pesa mfukoni, kisha wakaondoka mpaka nje ya wodi aliyokuwa amelazwa Taita na bahati nzuri walimkuta yule mama mtu mzima ambaye ni muuguzi,



"vipi mgonjwa anaendeleaje?" Sajenti Minja aliuliza baada ya kumsalimia,



"bado hali yake ni ile ile" Muuguzi alijibu,



"inaelekea alipigwa huyu kabla hajatupwa" Sajenti Minja aliongea,



"hivi baba, uliniambia mgonjwa ni nani yako?" Muuguzi alimuuliza Sajenti Minja,



"sina undugu nae, mimi ni askari tu nafuatilia tukio lililomkuta" Sajenti Minja aliongea huku akitabasamu,



"ooh kumbe ni askari?? sasa haya mambo ya watu kutekwa na kuokotwa naona yamepamba moto, au kuna biashara inafanyika?" Muuguzi aliongea huku Akimtazama Sajenti Minja,



"hakuna anayeyajua, inawezekana kati ya mtekwaji na mtekaji kuna namna walifanya biashara na kwa namna moja ikashindikana" Sajenti Minja alijibu huku akitabasamu,



"au kuna mtu ameingia hapa jijini na anateka tu watu hovyo?" Muuguzi alimuuliza Sajenti Minja,



"hata mimi sijui na ndio maana nafanya uchunguzi, inawezekana unayosema ni sawa, ila sisi kama polisi hatuwezi kuhisi kitu na kutangazia uma, ni lazima tuwe na uhakika na hicho kitu" Sajenti Minja aliongea huku akiona maswali ya muuguzi yanampa kero,



"unajua kwanini nakuuliza hivyo? Kuna mtu mwingine ambaye ameokotwa asubuhi hii" Muuguzi aliongea maneno yaliyomfanya Sajenti Minja ashtuke,



"ameokotwa eneo gani?" Sajenti Minja aliuliza,



"njia ya kwenda nje ya mji, alikutwa mtaroni" Muuguzi alijibu,



"ni mwanamke au mwanaume?" Sajenti Minja aliuliza,



"ni binti, ni daktari, wenzake walikuja na kudai ni daktari, na mwenzake mwingine ametoka hapa muda huu huu" Muuguzi aliongea



"aisee, nae hajakutwa na jeraha lolote mwilini?" Sajenti Minja aliuliza,



"amevunjwa miguu yote, yaani hapa kufikia mchana atakuwa kwenye chumba cha mifupa kwa ajili ya kutibiwa miguu" Muuguzi aliongea,



"yupo wodi namba ngapi?" Sajenti Minja aliendelea kuuliza,



"namba ishirini na tatu" Muuguzi alijibu na wakati huo Sajenti Minja akapiga hatua kuelekea kwenye mlango wa wodi, alipofika alisimama mlangoni na kumuangalia Dokta Pendo aliyekuwa amelala huku akiwa hana fahamu. Ila Sajenti Minja hakuweza kumtambua Dokta Pendo kutokana na mipira aliyovalishwa kwa ajili ya kumsaidia kupumua, na pia umbali ulichangia, kwa maana Sajenti Minja alisimama nje ya mlango na kumtazama Dokta Pendo kwa kupitia kioo kilichokuwepo mlangoni hapo.



"kuna polisi yoyote alikuja hapa kumuangalia zaidi yangu?" Sajenti Minja aliuliza,



"zaidi ya wale polisi waliomleta, hakuna mwingine aliyefika kumuona" Muuguzi alijibu,



"hii hatari sana, itabidi usalama uongezeke hapa, inawezekana kuna watu wabaya wanaweza kuja hapa" Sajenti Minja aliongea huku akiondoka eneo la mlango wa wodi aliyolazwa Dokta Pendo.



.

"suala la usalama linazingatiwa na ndio maana mimi nipo hapa" Muuguzi aliongea,



"kuna mtu yoyote alikuja kumuona huyu mzee?" Sajenti Minja aliuliza huku akinyooshea kidole katika Chumba cha wodi alicholazwa Taita.



"watu wengi wanakuja kumuona, tena mpaka viongozi wa serikali" Muuguzi aliongea,



"ni mtu mzito sana huyo" Sajenti Minja aliongea,



"ni nani?" Teja mmoja aliuliza,



"usikute tumemsaidia waziri mwanangu" Teja mwingine aliongea na kufanya Sajenti Minja na Muuguzi wacheke,



"twendeni bwana, mmeshaanza kelele zenu" Sajenti Minja aliongea huku akiondoka na kufanya wale vijana mateja wamfuate kwa nyuma na wakaondoka zao eneo lile la hospitali.



*********, ***



Sarah alivyotoka pale hospitali alielekea moja kwa moja kwenye gari lake na kuliondoa kwa kasi huku akiwaza wale mateja wamefuata nini pale hospitali?



"au wameitwa kunipeleleza? ila kama wamekuja kunipeleleza mbona hawatanifanya kitu baada ya kuniona? au hawajanijua?" Sarah alikuwa akijiuliza maswali na kujijibu mwenyewe,



"haya sasa kama hawajaja kunichunguza watakuwa wamefuata nini pale? lile eneo la wagonjwa mahututi uwa panahitajika usalama wa kutosha, sasa watu kama wale wamefuata nini pale? au Taita aliokotwa amelazwa pale?" Sarah aliendelea kuwaza huku akiwa anaendesha gari.



"sasa kama Taita atakuwa amepatikana akiwa hai itakuwaje sasa, nmefanya uzembe mkubwa kumuachia, ningejua ningefanya mabadilishano, ningewapa Taita na wao wangenipa babu yangu, sasa kwa hali ilivyo sasa siioni kama babu yangu atakuwa hai, ila kama angekuwa amekufa si wangemtupa kama Dokta Pendo, wangemtupa na watu wangemuokota. Nina imani babu yangu yupo hai ila sijajua suala la usalama wake wa mwili, isije kuwa wamemfanya kama Dokta Pendo" Sarah aliendelea kutafakari huku akijilaumu kwa mambo kadhaa,



"Dokta Pendo utapona shoga yangu, usijali utaishi kwa amani tu, hawa watu nitawamaliza mwenyewe, ahadi ya kisasi Lazima itimie, kisha na historia iandikwe na jina langu likumbukwe na vizazi" Sarah aliongea peke yake huku akaisimamisha gari nje ya geti lake, kisha akashuka na kufungua geti, akaingiza gari ndani ya geti.



************



Baada ya siku mbili, Nyakati za kumi jioni, Harry alikuwa uwanja wa ndege akionekana kumsubiri mtu. Baada ya dakika kumi mlango wa kutokea wageni ulifunguliwa, akatoka kijana mwenye umbo la wastani na pia ni mrefu wa futi sita na inchi 3, mgongoni alibeba begi la kijani na mkononi alikuwa na begi kubwa kiasi, alivaa suruali ya kitambaa nyeusi na shati la rangi ya bluu alilolichomekea vyema kwenye suruali yake hiyo, na chini alivaa viatu vyeusi, vinaitwa moka.



Harry alipomuona alimkimbilia na kumlaki kwa bashasha, yule kijana alijitahidi kutabasamu ila kiukwelie sura yake ilionesha hakuwa na furaha hata kidogo,



"Za safari Vin?" Harry alimsalimu,



"njema, za maisha?" Vin alijibu huku akiangaza angaza mazingira yaliyomzunguka,



"tunamshukuru Mungu, vipi umeshakula?" Harry aliuliza,



"hayo masuala ya kula yatafuata baadae, twende hospitali nikamuone baba" Vin aliongea,



"sawa bosi, twende kwenye gari" Harry aliongea huku akichukua begi mikononi mwa Vin na kushika njia iliyompeleka mpaka alipoegesha gari lake, akamfungulia mlango Vin, kisha Vin akaingia na yeye Harry akaenda upande wa dereva na kuingia, akawasha gari na kuliondoa kwa mwendo mdogo,



"Harry ujue kuna kitu unanificha, Baba yangu kwa ulinzi wake alionao alitekwaje, ni mtu gani alimteka?" Vin aliuliza huku macho yakiwa mbele,



"subiri mwenyewe ahamke, atakusimulia tu" Harry alijibu huku akijichekesha,



"na asipohamka ni nani atanielezea?" Vin alihoji huku akionekana mwenye hasira,



"usiseme hivyo, tuombe tu ahamke" Harry aliongea,



"iko hivi Harry, Baba asipohamka ni wewe ambaye utanieleza haya mambo, kwa hiyo sioni sababu ya kunificha sasa hivi, niambie tu" Vin alimshawishi Harry,



"sawa boss, ni hivi, hizi siku za karibuni baba yako pamoja na sisi ambao tupo chini yake tulipoteza kujiamini kabisa baada ya kuibuka mtu ambaye alikuwa akitufuatilia, mara ya kwanza hatukumchukulia kwa uzito mkubwa, ila alikuja kutuletea athari kubwa sana, aliua wenzetu si chini ya wawili, ameteketeza magari ya baba yako si chini ya mawili na ameshawahi kulipua geti la nyumba ya baba yako" Harry aliongea na kumfanya Vin amgeukie ili kumsikiliza vizuri,



"huyo mtu ana madai yoyote labda kutoka kwa baba?" Vin aliuliza,



"hakuna anayejua" Harry alijibu,



"hakuna anaejua vipi sasa? Wewe ukikaa na baba hamjawahi kulijadili hilo jambo?" Vin aliuliza kwa kufoka baada ya kuhisi Harry anataka kumchezea akili,http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



"ningekua najua ningekwambia tu, kwanini nikufiche mwanangu?" Harry aliongea kwa sauti ya upole,



"na anawauaje wenzenu, anawateka au anatumia nini?" Vin aliendelea kuuliza,



"aisee amejipanga, anatumia akili nyingi sana, pia ana mitambo ambayo anaweza kujua mtu alipo na akamfuatilia, pia ana simu ambayo anaweza kukupigia ila wewe ukimpigia inaonesha hiyo namba haipo na wala haikuwahi kutumika duniani" Harry aliendelea kutoa maelezo,



"Alafu ana nini kingine cha ziada tofauti na hivyo ulivyovitaja?" Vin alihoji,



"kingine ni mwanamke, tena sio mwanamke, ni kasichana tu kalichokuzidi miaka miwili" Harry aliongea huku macho yakiwa makini na barabara,



"msichana? inaelekea unamjua vizuri, mpaka umri wake umeujua?" Vin aliuliza huku akishangaa,



"ni huyo msichana mwenyewe uwa anajiweka wazi pindi anapokuja kutushambulia" Harry aliongea huku akiingiza gari yake eneo la hospitali,



"nadhani huyo msichana anastahili kufa, hawezi kumnyima raha baba yangu kiasi hiki na isitoshe tayari amemuweka katika hali mbaya kiafya" Vin aliongea huku akishuka katika gari,



"ngoja nitangulie kuingia ili kama nikikuta watu niwaondoe" Harry aliongea huku akipiga hatua za haraka haraka kuingia ndani ya eneo la hospital, na kumuacha Vin akielekea kwenye duka moja liliopo ndani ya uzio wa hospitali na kununua maji ya kunywa, kisha kwa mwendo wa taratibu Vin akawa anaelekea ndani ya jengo la hospitali huku akiwa anajaribu kujenga picha namna hali ya baba yake iliyokuwa.



Wakati Vin akiwa anaingia ndani ya eneo la hospital huku akiwa ana uchungu mkubwa juu ya hali ya baba yake na pia akiwa na hasira na msichana ambaye ameambiwa ndio aliyemtendea ubaya baba yake, ndio wakati huo huo msichana huyo ambaye ni Sarah alikuwa akitoka nje ya hospitali huku akiwa na uchungu mkuu dhidi ya Taita na watu wake baada kumfanyia ubaya Dokta Pendo ambaye mpaka leo bado hujapata fahamu.



Vin aliendelea kupiga hatua huku macho yakiwa mbele na wakati huo Sarah nae ndani ya baibui kubwa jeusi alikuwa akipiga hatua za haraka haraka za kutoka nje.



Na sasa walikuwa wanaelekeana, Vin alikuwa mbele ya Sarah na Sarah alikuwa mbele ya Vin, walikuwa wamebakiza hatua kumi tu kufikiana.



Zikiwa zimebaki hatua tano ili wafikiane, Vin akanyanyua uso wake na kumuangalia Sarah, ghafla tu mapigo ya moyo wake yakabadilika na kuanza kwenda mbio huku moyoni hali fulani ya mshtuko ikimtawala, wakati Vin hali hiyo ikimtazama, kwa upande wa Sarah alihisi kama huyo kijana akimuangalia na yeye ikabidi amtupie jicho, hapo sasa nae Sarah ikamkuta hali ile ile, tena mbaya zaidi mpaka machozi yakawa yanataka kumtoka ila alijizuia huku akishangaa kwanini akutane na hali kama ile?



Walisogeleana mpaka wakawa wanakaribia kupishana, walipopisha Sarah akapiga hatua moja akasimama, Vin nae akahisi yule dada waliyekuwa wakiangaliana amesimama, Vin akasimama huku wakiwa wamepeana migongo na kila mmoja akishangaa ni kwanini hiyo hali imetokea?



Wakiwa bado wamesimama huku wamepeana migongo, ndipo Harry alitokea kwa mbele ya Vin, nyuma ya Sarah. Alikuwa mbali kidogo, ila alipotokea na kuona hilo tukio alisimama ghafla na kutazama, kisha akaamua aanze kusogea jirani na Vin na kipindi anasogea, Sarah hakuwa na habari na hilo, yaani hakuwa akijua kama Harry anajongea eneo lile, Sarah aliendelea kusimama tu huku akijishangaa ile hali iliyomkuta...........







Wakati Vin na Sarah wakiwa wamesimama huku wote wakiwa kimya na hakuna aliyekuwa anamuangalia mwenzake, na kipindi hicho Harry nae aliongeza mwendo ili kufika eneo la tukio.



Sarah akaanza kupiga hatua za haraka kuelekea nje, alitembea mpaka katika gari yake na kuingia,



"kwanini moyo wangu umekuwa na hisia nzito juu ya yule kijana?" Sarah alijiuliza huku akiiondoa gari yake kutoka nje ya geti la hospitali na kujaribu kupuuza hisia zisizoeleweka juu ya kijana yule, kitu ambacho hakukijua ni kuwa yule kijana ndiye mdogo wake ambaye hakuwahi kujua ni wapi alipo.



Sarah alielekea moja kwa moja mpaka eneo moja katikati ya mji na kwenda kusimamisha gari yake mbele ya kijiwe kimoja ambacho kilikuwa na watu wa rika mbalimbali wakicheza michezo tofauti kama bao, drafti, na karata, aliposimamisha gari akaangaza macho na kumuona mtu aliyekuwa alimuhitaji, Sarah akapiga honi kisha watu wengi wakageuka kumuangalia mpiga honi, wengi wao baada ya kumuangalia Sarah walirudisha macho yao mbele kuendelea na kazi zao, isipokuwa yule kijana muhusika alipogeuka na kumuona Sarah, aliweka karata chini na kukimbilia kwenye gari la Sarah, alipofika aliingia ndani ya gari,



"sema bosi?" kijana aliongea,



"poa, ndio nimekuja tukaione hiyo nyumba" Sarah aliongea,



"sawa twende" kijana aliongea kisha Sarah akaondoa gari kuelekea kwenda kwenye hiyo nyumba.



"unataka ukaishi wewe?" kijana alimuuliza Sarah,



"kuna babu yangu nataka akaishi uko" Sarah alijibu,



"kwa sasa anaishi wapi?" Kijana ambaye alikuwa ni dalali aliuliza,



"yupo tu, tunaishi nae" Sarah alidanganya,



"ila dada kule ulipopachagua ni mbali, ni nje ya mji kabisa" Kijana aliongea,



"panamfaa kule, maana ni mzee na isitoshe gharama za ndogo za ununuzi wa hiyo nyumba" Sarah aliongea,



"kwa hizo sababu ni sawa. Mzee ataishi peke yake au yupo na mkewe?" Kijana aliuliza, huyu kijana alikuwa na maneno mengi sana,



"yupo kundi kubwa tu la kuishi nalo, ana timu ya mpira" Sarah alijibu na kuwafanya wote wacheke na kipindi hicho gari ilikuwa inasimama nje ya nyumba moja ambayo ilikuwa na uzio bila geti, ila nyumba ilikuwa imekamilika yote, ilikuwa haijapakwa rangi tu.



Sarah baada ya kutelemka katika gari, alianza kuikagua ile nyumba, alianza kwa kuizunguka eneo la nje, baada ya kuridhika akaingia ndani na kuanza kuzungukia kila chumba, baada ya kujiridhisha walitoka mpaka eneo la nje,



"ndio ulisema inauzwa shilingi ngapi?" Sarah alimuuliza kijana dalali,



"anataka million themanini na moja" Dalali alijibu,



"hivi ukiniangalia unaniona nimekaa kitajiri eee? au mgeni sana wa jiji?" Sarah alimuuliza dalali huku akitabasamu,



"kwanini unasema hivyo boss?" Dalali aliuliza,



"hii nyumba sio ya million themanini, mimi nitatoa hamsini, kama haiwezekani ni basi, maana ndiyo iliyopo" Sarah aliongea huku akikaa juu ya tofali lililokuwepo hapo,



"bosi uko unanyonga sana, OK, fanya Sabini na tano" Dalali aliongea,



"Mimi nadhani huanielewa, mimi ninayo hamsini tu. Kama haiwezekani basi biashara ife" Sarah aliongea kwa nyodo huku akimtazama,



"basi kusema kweli kabisa, hii nyumba ni million sitini, zaidi ya hapo haishuki" Dalali aliongea kiunyonge na kumfanya Sarah amcheke,



"hiyo ndiyo bei halali sasa, sasa nitakupa sitini na moja" Sarah aliongea na kumfanya dalali ashangae mwenyewe huku akicheka,



"mbona hueleweki bosi, nikipunguza bei, wewe unaongeza" Dalali aliongea,



"nadhani tangu mwanzo ungeanza na hiyo bei, ungenielewa" Sarah aliongea huku akitabasamu,



"sawa bwana, sasa kuhusu suala la malipo ni mpaka kesho nitakapokukutanisha na mwenye nyumba, muda gani utakuwa free?" Dalali alimuuliza Sarah,



"nitakupigia simu jioni" Sarah alijibu huku akielekea kwenye gari lake,



"sawa bosi, nakuaminia" Dalali aliongea huku nae akielekea kupanda katika gari ya Sarah.



**********************



Vin aliendelea kusimama pale pale, alisikia wakati Sarah akiondoka ila hakutaka kumuangalia, aliendelea kuganda vile vile mpaka Harry alipomfikia,



"mbona hivyo, yule msichana uliyesimama nae unamjua?" Harry alimuuliza Vin,



"Hapana, ni nani?" Vin aliuliza,



"Mimi sijui ndio maana nimekuuliza wswe" Harry aliongea ukweli kwa maana hakumuona kweli Sarah,



"twende, achana nae" Vin aliongea huku akianza kupiga hatua,.



"labda ni malaya tu anataka kukurubuni" Harry aliongea huku nae akimfuata Vin,



"ataniweza sasa? mimi ni mtu ninaejielewa" Vin alijibu huku moyoni akiwa anashangaa ni kwanini moyoni amekuwa mzito baada ya kumuona yule msichana, tena msichana mwenyewe ndio amemuona kwa mara ya kwanza.



"nakuaminia mzee, uko marekani kuna warembo zaidi ya hapa" Harry aliongea huku akijichekesha mbele ya Vin,



"kwetu wanawake ni warembo zaidi" Vin aliongea huku wakiwa wameifikia wodi namba ishirini na moja ambayo ndiyo alikuwa amelazwa Taita. Vin akataka aingie moja kwa moja ndani ya wodi ila yule mama mtu mzima ambaye ni muuguzi, alimzuia,



"haruhusiwi mtu kuingia ilipokuwa Dokta tu" Muuguzi aliongea huku akimshika bega Vin, Vin akasimama huku akimuangalia kwa mbali baba yake, baada ya dakika moja machozi yalikuwa yakitiririka kwenye mashavu ya Vin, alimpenda sana baba yake huyo, na hapo alikuwa akilia huku akimuomba Mungu ampe uhai zaidi baba yake,



"jikaze, atapona tu" Muuguzi aliongea huku akiwa amesimama nyuma ya Vin, Vin akageuka na kumuangalia Muuguzi,



"atapona? wewe unaijua mipango ya Mungu?" Vin alimuuliza Muuguzi huku akiwa na hasira,



"tulia Vin, twende ukapumzike, utarudi baadae" Harry aliongea kinyenyekevu mbele ya Vin na kipindi hicho Muuguzi alikuwa ameogopa na alikaa mbali kabisa,



"sipendagi mtu aongee vitu ambavyo havijui" Vin aliongea huku akianza kuondoka na Harry alikuwa nyuma yake,



"mama tusamehe, endelea kuangalia usalama" Harry aligeuka na kumwambia Muuguzi na kisha akaendelea kusonga mbele kumfuata Vin.



*************************



Baada ya wiki, Dokta Pendo alikuwa amezinduka na alijikuta ana bandeji ngumu kwenye miguu yake yote miwili na wodi alikuwa amehamishwa, alihamishiwa kwenye wodi za kawaida.



Sajenti Minja alifika hospitali pale na kuelekea moja kwa moja kwenye wodi za watu mahututi na kumuona Taita, kisha yule mama Muuguzi akampa taharifa za kuhamishwa kwa Dokta Pendo, Sajenti Minja akaulizia ni wapi alipohamishiwa, akaelekezwa na kwenda moja kwa moja kwenye hiyo wodi, haukuwa muda wa kuangalia wagonjwa ila alijitambulisha yeye ni askari na ameenda pale kikazi, akaruhusiwa kuingia.



Alipoingia na kumuona mgonjwa mwenyewe ilibidi ashangae kwa maana anamfahamu,



"Pendo, vipi?" Sajenti Minja aliongea huku akikaa pembezoni mwa kitanda,



"salama kiasi, karibu" Dokta Pendo aliongea kwa tabu huku miguu yake ikiwa imetundikwa juu,



"nini tatizo tena?" Sajenti Minja aliuliza,



.



"nilitekwa ndugu yangu, kwanza kujikuta mzima hivi nimeshangaa, mi nilikuwa mtu wa kufa" Dokta Pendo aliongea,



"walikuteka unawajua? au sababu za kukuteka unazifahamu?" Sajenti Minja aliuliza,



"kuwajua nawajua kwa sura, ila sababu ya kuniteka ni yule mwanamke uliyekuwa unamfuatilia na niliyekuja kutoa taharifa kuwa aliniteka hawali" Dokta Pendo aliongea,



"kwanini wakuteke wewe na sio yeye?" Sajenti Minja aliuliza,



"waliniteka mimi wakitaka iwe njia ya kumpata yeye, waliamini tuna urafiki na mawasiliano" Dokta Pendo aliongea,



"na ulisikia wakiongea kitu chochote kumuhusu huyo dada?" Sajenti Minja aliuliza,



"waliongea vingi tu ikiwemo kuwa wakimpata lazima wamuue" Dokta Pendo aliongea,



"na huyo dada unavyomjua wewe ni kweli ni mtu mbaya?" Sajenti Minja aliuliza,



"ni mtu mbaya, wewe mwenyewe si ameshawahi kukushambulia? Kwanza namchukia kwa maana yeye ndio amenisababishia mambo yote haya, ameniharibia maisha na sasa siwezi kufanya kazi na nina watu wananitegemea" Dokta Pendo aliongea kwa uchungu huku machozi yakimtoka,



"pole, na tangu muda umehamishiwa hapa, huyo dada amekuja kukuona?" Sajenti Minja aliuliza,



"sitaki hata aje, ni shetani kama inawezekana nipe hata bastola ili akija nimmalizie mbali" Dokta Pendo aliongea kwa chuki huku akiwa bado analia,



"pole sana Dokta, ilo suala lako ngoja nilifuatilie mimi kwa ukaribu zaidi" Sajenti Minja aliongea huku akimfuta machozi Dokta Pendo,



"yaani kila sura yake ikija kichwani kwangu napata maumivu, yaani ameniharibia maisha mbwa huyu" Dokta Pendo aliendelea kulalamika kwa kilio cha kwikwi,



"usijali Dokta, mchana huu unataka ule nini?" Sajenti Minja alimuuliza,



.

. "saa ngapi kwani?" Dokta Pendo aliuliza huku akifuta machozi,



"saa saba na nusu" Sajenti Minja alijibu,



"muda wa kuona wagonjwa umefika, sasa hivi naletewa chakula kwa hiyo usisumbuke kutumia pesa yako" Dokta Pendo aliongea na muda huo mlango wa wodi ulifunguliwa na akaingia yule mama Muuguzi,



"nimekuletea mgeni" Muuguzi aliongea huku akitabasamu na nyuma yake akaingia Sarah huku akiwa na tabasamu pana usoni mwake ila Dokta Pendo alihamaki na sura yake ikaonesha hasira zaidi........







"ngoja kwanza niongee, kati ya watu walikuwa wanalia kila wakikuona ni huyu hapa, ni mtu ambaye muda wote alikuwa nje ya wodi, kama ni rafiki huyu ni rafiki bora" Muuguzi aliongea kwa kumpa sifa Sarah huku akitabasamu,



"Sarah karibu, kumbe mnajuana na Pendo?" Sajenti Minja aliongea huku nae akitabasamu na kumfanya Dokta Pendo ashangae kumbe Sarah na Sajenti Minja wanajuana,



"asante sana" Sarah alijibu kwa furaha huku machozi yakimtoka, akaelekea alipo Dokta Pendo na akampiga busu katika paji la uso wa Dokta Pendo, Dokta Pendo hakuwa na furaha ila kwa maelezo aliyoyasikia kutoka kwa yule mama Muuguzi, roho ya imani ilianza kumuingia Dokta Pendo, akajikuta chuki aliyonayo juu ya Sarah ikipungua taratibu,.



"pole shoga yangu" Sarah aliongea huku akimuangalia Dokta Pendo,



"asante" Dokta Pendo alijibu huku akionekana hana furaha,



"mbona huna furaha shoga yangu, au hukupenda ujio wangu?" Sarah aliuliza huku akitabasamu,



"furaha itatoka wapi na ulemavu huu?" Dokta Pendo aliuliza huku huzuni ukizidi kumtawala,



"utapona tu, hayo ni matatizo ya kawaida mwanangu" Muuguzi aliongea huku akielekea nje,



"ngojeni niwaache kidogo, nitarudi baadae" Sajenti Minja nae aliongea huku akielekea nje na kumuacha Dokta Pendo na Sarah ndani ya wodi.



"nikakununulie nyama shoga yangu?" Sarah alimuuliza Dokta Pendo,



"hapana, najihisi kushiba" Dokta Pendo alijibu,



"naweza kukuuliza kitu?" Sarah aliongea huku akimkazia macho Dokta Pendo,



"niulize tu" Dokta Pendo aliongea,



"najua waliokuteka ni kundi la Taita, je umeshapajua wanapoishi?" Sarah alimuuliza Dokta Pendo,



"hapana Sarah, mimi sitaki tena kujihusisha na mambo yenu" Dokta Pendo aliongea huku akigeuza shingo pembeni,



"hapana, sio kwamba nataka nikuhusishe, nataka nikusaidie" Sarah aliongea huku akiwa bado anamtazama Dokta Pendo,



"unisaidie nini tena wakati nimeshatoka mikononi kwo?" Dokta Pendo aliuliza,



"bado hujatoka, ni lazima wakumalize wakigundua upo hai" Sarah alimtahadharisha,



"hawawezi, kwanza hili suala nimeshamwambia huyu askari tuliyekuwa nae hapa" Dokta Pendo aliongea na kumfanya Sarah ashtuke,



"sasa hata kama umemwambia, atawajuaje au atawapata wapi hao waarifu?" Sarah alimuuliza,



"tatizo sio waarifu, nimemwambia kwa ajili ya ulinzi wangu tu" Dokta Pendo alijibu,



"sasa huyu atakusaidia nini wakati mimi peke yangu namshinda, ataweza kukulinda dhidi ya kundi kubwa?" Sarah aliuliza huku akimshamshangaa,



"potelea mbali, alafu kingine naomba ukae mbali na mimi, tena nakuomba kwa mikono miwili" Dokta Pendo aliongea huku akimaanisha anachokizungumza,



"nitakaa tu mbali na wewe, ila baada ya kuhakikisha upo salama" Sarah aliongea na wakati huo Sajenti Minja alikuwa akiingia ndani ya wodi hiyo,



"muda wa kuangalia wagonjwa umeisha, Sarah bado upo?" Sajenti Minja aliuliza huku akitabasamu,



"kumbe muda umeisha? Mimi bado natamani kukaa na shoga yangu" Sarah aliongea huku akionesha huzuni usoni, na kipindi hicho mfanyakazi mmoja wa hospitali aliingia na kuwahimiza Sarah na Sajenti Minja watoke ndani,



"usiku ni muda gani ndio wagonjwa wanaangaliwa?" Sarah alimuuliza mfanyakazi wa hospitali,



"ni saa moja na nusu mpaka saa tatu" Mfanyakazi wa hospitali alijibu,



"nitakuja muda huo" Sarah aliongea huku akitoka nje,



"Pendo, nitakuja muda wowote tuongeee, ngoja niongee kidogo na Sarah" Sajenti Minja aliongea,



"sawa haina shida" Dokta Pendo alijibu na kumfanya Sajenti Minja nae aende zake nje kumuwahi Sarah.



Sajenti Minja akatoka mpaka nje na kumkuta Sarah tayari ameshaingia ndani ya gari lake, Sajenti Minja akaenda kwenye upande wa kioo cha pili na kugonga, Sarah akakitelemsha kioo na kumuona Sajenti Minja, Sarah akatabasamu,



"vipi?" Sarah alimuuliza Sajenti Minja,



"toa lock niingie, au hutaki?" Sajenti Minja aliuliza huku akitabasamu kisha Sarah akatoa lock na Sajenti Minja akaingia ndani ya gari.



"nambie mrembo, za siku?" Sajenti Minja alimtakia hali Sarah,



"safi, za kunisusa?" Sarah alijibu huku akitabasamu,



"nipo bize sana, si unajua kazi zetu hizi" Sajenti Minja aliongea,



"sawa bwana, mimi nipo" Sarah alijibu,



"naomba unisaidie kitu, Dokta Pendo ana rafiki ambaye ndiye anayesababisha matatizo yote haya, sijui unamjua huyo rafiki yake?" Sajenti Minja swali lililomuogopesha Sarah



"hapana simjui, ningekuwa namjua nadhani ningeshawataharifu polisi" Sarah alijibu huku akiwa na wasiwasi,



"nadhani ni yule mwanamke aliyekushambulia siku ile Vin hotel" Sajenti Minja aliongea,



"labda, ila yule mwanamke simjui na pale ndio nilimuona kwa mara ya kwanza na sura yake sikuweza kuikariri kutokana na giza" Sarah alijibu,



"Dokta Pendo kinachomponza anashindwa kuwa muwazi, hicho ni kitu kibaya sana, hicho kitu kinaweza kusababisha matatizo makubwa zaidi" Sajenti Minja aliongea huku akisikitika,



"inawezekana amechanganyikiwa muda huu, ngoja akili yake itulie kidogo labda anaweza kukueleza vyote anavyovijua" Sarah aliongea huku akibofya simu yake,



"nikishamjua huyo mwanamke na nikajua lengo lake, nadhani nitakuwa nimepiga hatua muhimu sana" Sajenti Minja aliongea huku akitazama mbele,



"nina imani Kama utatuliza akili na kama Dokta Pendo atakupa ushirikiano wa kutosha, lazima utamjua" Sarah aliongea huku akimuangalia kwa makini Sajenti Minja,



"kwa umakini nipo makini, ila lazima nipate ushirikiano wa kutosha" Sajenti Minja aliongea,



"Alafu kitu kingine, usichukulie huyo mwanamke katika upande mbaya tu, lazima umfikirie mara mbili, huenda kuna kitu kizuri anakifanya" Sarah aliongea huku akiwa ameangalia chini,



"yote unayosema ni sawa, ila kama angekuwa na lengo zuri si angejitokeza kwenye vyombo vya usalama?" Sajenti Minja aliuliza,



"kwani ukimuona unamjua?" Sarah alimuuliza Sajenti Minja,



"hapana" Sajenti Minja alijibu huku akimuangalia Sarah,



"basi huenda ameshajitokeza sana kwenye vyombo vya usalama, au huenda ameshawahi kuwa mbele yako ila ukashindwa kumtambua" Sarah aliongea na kwa maana hiyo alikuwa anajiweka wazi mbele ya Sajenti Minja ila alijiweka kwa njia ya fumbo.



"unachoongea ni kweli, mimi nitajitahidi kumchunguza Dokta Pendo, na wewe naomba ujitahidi kumchunguza rafiki yako ili tuweze kumsaidia" Sajenti Minja aliongea huku akimuangalia Sarah,



"usijali afande, nitafanya hivyo. Naomba niondoke sasa" Sarah aliongea huku akiwasha gari,



"mbona unawahi hivyo?" Sajenti Minja aliuliza,



"Kuna kazi muhimu naiwahi" Sarah alijibu,



"poa, lini nije nikutembelee kwako?" Sajenti Minja aliuliza,



"siku yoyote tu utakayojisikia, cha muhimu mawasiliano" Sarah alijibu,



"poa tutawasiliana mrembo" Sajenti Minja aliongea huku akitabasamu,



"poa, tchao handsome boy" Sarah aliongea kisha akaiondoa gari yake na kumuacha Sajenti Minja akiiangalia huku akitabasamu peke yake.



****************



Ndani ya Vin hotel kulikuwa na majadiliano baina ya watu watatu, Harry, Vin na Trigger.



"kwani kwa ukaribu wako wewe na mzee, hajawahi kukwambia kitu chochote kumuhusu huyo Sarah?" Vin alimuuliza Harry,



"hajawahi kuniambia kitu, labda huyo umuulize" Harry aliongea huku akinyooshea kidole kwa Trigger,



"na huyu ni nani?" Vin aliuliza huku akimtazama Trigger,



"huyu ni mlinzi wa mzee, muda mrefu yupo nae" Harry alijibu,



"hata ile siku Taita anatekwa, nilikuwa nae" Trigger aliongea huku akijichekesha,







"sasa kama ulikuwa nae alitekwaje na wewe mlinzi ukiwepo, ni uzembe mkubwa sana, hutakiwi kuendelea kuwa mlinzi wa mzee" Vin alifoka kwa hasira,



"ujue siku ya tukio hakuna aliyotegemea mzee atatekwa, ila nilijitabidi na kumfikia adui, ila mzee akazuia nisifanye shambulizi kwa ajili ya usalama wake" Trigger alijitetea,



"huyo mwanamke mmeshakutana mara ngapi?" Vin alimuuliza Trigger,



"hiyo ilikuwa ni mara ya kwanza, ila nilikuja kukutana nae mara ya pili baada ya kufuata pesa ambazo mzee alidai nimpatie huyo mwanamke" Trigger alijibu,



"sawa, Harry mimi naona mzee bora nimpeleke akatibiwe marekani tu" Vin aliongea huku akimtazama Harry,



"ni wazo zuri, kwanini tusisubiri fahamu zimrejee kwanza?" Harry aliuliza,



"nadhani tungoje fahamu zimrudie" Trigger aliongea kumuunga mkono Harry,



"sioni kinachofanyika pale hospitali, mzee kakaa zaidi ya wiki na hata hajitingishi, kuna kupona kweli hapo?" Vin aliuliza kwa ukali,



"ujue zile drip wanazomtundikia ni kwa ajili ya kumuondoa sumu na kumuongezea nguvu, naimani ataamka tu" Harry alijibu,



"Dah, hivi huyo Sarah ni nani mpaka awaendeshe wanaume wenye akili na nguvu?" Vin aliuliza kwa hasira,



"utamuona tu, tuombe uzima" Trigger alijibu,



"nitamfanya vibaya, bora nisimuone tu" Vin aliongea na kisha akachukua glass ya maji na kuipeleka kinywani,



"Mimi ngoja niwaache, naenda ofisini mara moja" Harry aliongea huku akinyanyuka,



"usiku si utakuja kunipitia ili twende hospitali?" Vin alimuuliza,



"utaenda na Trigger, mimi na wewe tutakutana uko uko" Harry alijibu,



"sawa boss" Vin alijibu na kisha akaondoka zake,.



************



Nyakati za usiku, Trigger akiwa na Vin ndani ya gari walikuwa wakiegesha gari nje ya eneo la hospital, kisha wakatelemka,



"Boss wewe nenda, mimi nitakuwa hapa nje" Trigger aliongea huku akimuangalia Vin,



"kwanini sasa?" Vin aliuliza huku akishangaa,



"nataka nivute kwanza sigara, nitaingia muda si mrefu" Trigger alijibu,



"sawa, acha mimi nitangulie" Vin aliongea na kisha akaelekea ndani ya jengo la hospitali na kujaribu kumuacha Trigger akiwa amesimama pale nje, kitu kilichomfanya Trigger asiingie hospitali haikuwa ni sigara, ilikuwa ni ile Range Rover nyeusi iliyokuwa imeegeshwa nje ya jengo la hospitali, aliifananisha na gari ya Sarah ingawa hakuwa na uhakika nayo, ila aliamini itakuwa ni yenyewe kabisa,



"huyu malaya kama ni kweli ni yeye, atakuwa amefuata nini huku? Au ameshajua Taita yupo hapa na amekuja kummaliza?" Trigger alikuwa akijiuliza kisha akapiga hatua za haraka haraka kuelekea kwenye mlango wa lile jengo ambao ulikuwa ni wa kioo, ila kabla hajausukuma aliweza kumuona Sarah kupitia kioo, Sarah nae alikuwa anatoka ndani na kuja kwenye ule mlango wa jengo, ina maana Sarah alikuwa akaelekea nje.



Trigger ilimbidi atoke mbio mpaka kwenye gari la Sarah, na kisha akakitoa kidude fulani mfukoni na kukiweka kwenye kitasa cha gari, lock zikaachia, Trigger akafungua mlango na kuingia siti za nyuma, akalala nyuma ya siti.



Sarah akiwa hana hili wala lile, aliweza kutoka nje ya jengo la hospitali, alipolikaribia gari lake akatoa funguo na kobonyeza kisha gari ikapiga alarm ndogo za kutoa lock, Sarah akafungua mlango na kuingia, akatazama simu yake na kisha akaiweka siti ya pembeni yake, Sarah akawasha gari na kuiondoa usiku huo huku akiwa hajui kama Trigger yupo siti ya nyuma yake...................





Sarah aliendelea kuendesha gari huku akiwa hana habari kabisa kama kuna mtu siti ya nyuma, na wakati huo Trigger hakuwa na haraka ya kumdhuru Sarah, alichotaka ni kupajua nyumbani kwa Sarah na ikiwezekana Kama ni kumdhuru, basi amdhuru uko uko.



Wakati Sarah akiendelea kuendesha gari, alisimamisha gari ghafla, Trigger akashuka ila hakutaka kufanya papara, Sarah k akakunja kushoto na kuegesha gari nje ya mgahawa, akatelemka na kuingia ndani ya mgahawa, tena akachagua kiti kilichopo dirishani ili aiangalie gari yake,



"karibu dada, nikuhudumie nini?" Muhudumu alifika na kuuliza,



"ngoja kidogo, nitakuita" Sarah alijibu huku akiitoa simu yake mfukoni, akaibonyeza sehemu yenye majina na kuchagua jina alilonakiri kwa jina "AFANDE" akapiga, ilikuwa ni namba ya Sajenti Minja,



"hallow afande, upo wapi?" Sarah aliuliza baada ya simu kupokelewa,



"naelekea hospital, wewe upo wapi?" Sajenti Minja aliuliza,



"nipo overview restaurant, nina tatizo afande" Sarah aliongea huku macho yakiwa kwenye gari lake,



"tatizo gani tena mrembo?" Sajenti Minja aliuliza kwa shahuku ya kutaka kujua,



"ndani ya gari langu kuna mtu, nahisi aliingia kipindi mimi nipo wodini" Sarah aliongea na kusubiri,



"amejua kama umejua uwepo wake ndani ya gari?" Sajenti Minja aliuliza,



"bado hajajua" Sarah alijibu,http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



"nakuja hapo overview, jitahidi asijue kama umejua" Sajenti Minja aliongea,



"poa, fanya fasta" Sarah alijibu na kukata simu, kisha akaangaza macho na kumuita muhudumu wa mgahawa,



"niletee sambusa mbili na juisi" Sarah aliagiza kisha akainuka na kuelekea sehemu ya kusafishia mikono, baada ya muda mfupi alirudi na kukuta alichokiagiza kipo mezani, Sarah akaanza kula huku macho yake yakiwa kwenye gari lake, baada ya dakika tano, Sarah aliweza kuiona gari ya Sajenti Minja ikiegeshwa pembeni ya gari yake, Sarah akainuka kwenye kiti na kumuita muhudumu, kisha akampatia malipo yake na Sarah akatoka nje haraka haraka kumuwahi Sajenti Minja,



"yupo wapi" Sajenti Minja aliuliza huku akimtazama Sarah,



"mlango wa nyuma" Sarah alijibu,



"toa lock" Sajenti Minja aliongea huku akiitoa bastola yake. Sarah akatoa lock kwa kutumia remote ndogo iliyoambatanishwa na funguo ya gari.



Sajenti Minja kwa umakini mkubwa alifungua mlango wa gari na kunyooshea bastola, lakini hakukuta mtu,



"mbona hakuna mtu?" Sajenti Minja aliuliza na kumfanya Sarah ashtuke,



"atakuwa ameshakimbia, itakuwa alishtukia mchezo" Sarah alijibu,



"kweli maana naona mchana wa nyayo za viatu hapo kwenye siti. Aliingiaje na ametokaje?" Sajenti Minja aliuliza,



"Mimi sijui bwana" Sarah alijibu,



"ila nadhani atakuwa maeneo haya haya anakufuatilia" Sajenti Minja aliongea,



"inawezekana" Sarah alijibu,



"uligunduaje kuna mtu ndani?" Sajenti Minja aliuliza,



"nilisikia harufu ya perfume na pia nilihisi kuna kitu kama kinagusa gusa siti" Sarah alijibu,



"sasa ni bora nikusindikize nyumbani kwa ajili ya usalama" Sajenti alimwambia Sarah,



"Acha tu, nitafika" Sarah alijibu,



"hapana, panda kwenye gari mimi nitakuja kwa nyuma" Sajenti Minja aliongea,



"yes sir" Sarah alijibu huku akipiga saluti na pia akicheka,



"mjinga kweli wewe, unafurahi huku una matatizo" Sajenti Minja aliongea huku akicheka,



"sio tatizo hilo, kwangu ni kitatizo tu" Sarah aliongea huku akiingia kwenye gari lake,



"kingekuwa kitatizo usingeniita" Sajenti Minja aliongea huku akiwa bado anacheka,



"twende bwana, acha maneno yako" Sarah aliongea huku akiwasha gari yake na kipindi hicho Sajenti Minja alikuwa akielekea kwenye gari yake.



Sarah baada ya kuwasha gari yake, akakitoa kifua kidogo na kugeukia siti ya nyuma na kuanza kukagua kwa kutumia hicho kifaa, alikuwa anaangalia hali ya usalama, baada ya kujiridhisha aliondoa gari na huku nyuma akifuatwa na Sajenti Minja.



Iliwachukua dakika kumi kufika nyumbani kwa Sarah, Sarah akafungua geti na kuingiza gari yake, Sajenti Minja yeye gari aliiweka nje ya geti.



"karibu afande" Sarah aliongea huku akifungua mlango na kisha Sajenti Minja akaingia na kuksribushwa na mandhari nzuri ya sebule ya Sarah,



"asante sana, ni pazuri sana" Sajenti Minja aliongea,



"unatumia kinywaji gani?" Sarah alimuuliza,



"bia" Sajenti Minja alijibu huku akikaa kwenye kochi,



"bia hamna, kama unataka pombe kuna whusky" Sarah aliongea huku akitabasamu,



"basi nipe chochote ila sio pombe" Sajenti Minja aliongea kisha Sarah akamletea juisi tu.



"unaishi na nani hapa?" Sajenti Minja aliuliza,



"mwenyewe tu" Sarah alijibu huku akijitupa kwenye kochi,



"unaishiji mwenyewe kwenye kubwa hivi, huogopi?" Sajenti Minja aliuliza,



"niogope nini sasa?" Sarah aliuliza,



"inatakiwa ukae na mwenzako, au amesafiri unanidanganya tu?" Sajenti Minja aliuliza,



"naishi peke yangu bwana, mbona maswali mengi afande?" Sarah aliuliza huku akitabasamu,



"huwezi jua, labda nataka uwe mke wa afande" Sajenti Minja aliongea na kufanya wacheke,



"suala la kuolewa kwa muda huu sifikirii, maana kuolewa ni kuwa mtumwa wa ndoa, nitashindwa kukamilisha ndoto zangu" Sarah aliongea huku akitabasamu,



"ndoto gani uliyoibakiza? maana maisha mazuri tayari unayo" Sajenti Minja aliuliza,



"ndoto si kuwa na maisha mazuri tu, ndoto ni kukamilisha kile ulichopanga kukifanya kipindi upo mtoto" Sarah alijibu,



"kwa hiyo wewe ndoto yako ni nini?"Sajenti Minja aliuliza,.



"ninayo tu moyoni mwangu, nikiikamilisha nitakwambia" Sarah alijibu,



"sawa mama, acha nirudi hospitali, ila kuwa muangalifu na usalama wako" Sajenti Minja aliongea huku akisimama,



"mbona unaondoka hata juisi haijaisha?" Sarah aliuliza kwa mshangao,



"utamalizia wewe mke wa afande" Sajenti Minja aliongea huku akicheka,



"sawa bwana, mimi hata sikutoi" Sarah aliongea,



"geti nani atafunga?" Sajenti Minja aliuliza,



"rudishia tu" Sarah alijibu na kisha Sajenti Minja akaondoka zake.



Sarah akabaki sebuleni peke yake huku akitafakari ni nani yule aliyeingia kwenye gari yake.



"atakuwa ameingia pale pale hospitali, na walikuwa wananifuatilia, haiwezekani wajue nipo pale, sasa kama watakuwa wamejua pale ninaenda kwa ajili ya kumuona Dokta Pendo, basi hali ya Dokta Pendo itakuwa matatani sana" Sarah aliongea huku akielekea nje kufunga geti.



****************



Trigger wakati yupo, kwenye gari la Sarah, alipata wasiwasi baada ya kumuona Sarah akiongea ndani ya mgahawa na Sajenti simu, wasiwasi uliongezeka zaidi baada ya kumuona Sajenti Minja, maana alikuwa anamjua. Alichofanya Trigger ni kuchomoka kwenye gari na kuondoka zake. Safari yake iliishia hospitali, alipofika alimkuta Harry, ikabidi amtoe nje wakaongee,



"Sarah ametoka hapa muda si mrefu" Trigger aliongea huku akimtazama Harry,



"amefuata nini hapa?" Harry aliuliza,



"Labda bado anamfuatilia Taita, anataka ammalize" Trigger alijibu,



"huenda, ebu imarisheni ulinzi kote, ikiwezekana ongeza vijana wawe eneo la nje ya hospitali" Harry aliongea,



"sawa mkuu, je tumshirikishe Vin juu ya Sarah kuonekana hapa?" Trigger aliuliza,



"hilo suala niachie mimi" Harry alijibu,



"sawa, acha mimi nizunguke zunguke eneo hili la hospitali kuangalia usalama zaidi" Trigger aliongea,



"sawa" Harry alijibu huku akiondoka zake na kumuacha Trigger nae akigeuka na kuondoka zake.



Trigger aliamua kuzunguka tu ndani ya hospitali, hiyo ziara ya ghafla aliita ziara ya kukagua usalama. Wakati Trigger akiwa anapita maeneo tofauti ndani ya hospitali, ndipo alipopita katika wodi moja iliyompa mshtuko, hiyo wodi ndipo aliyolazwa Dokta Pendo, Trigger ilimbidi asimame pale kwa sekunde kadhaa kwa ajili ya kuhakikisha anachokiona, baada ya kujiridhisha, alitoka mbio mpaka alipo Harry, akamtoa nje,



"kuna hatari, yule mwanamke Dokta tuliyemteka na kumtupa, yupo hapa, amelazwa" Trigger aliongea huku akihema juu juu,



"basi itakuwa Sarah ndio alikuja kumuona na ndio maana mkaonana" Harry aliongea,



"hili ni tatizo, wewe unadhani huyu demu akipona itakuwaje, si lazima atatoa taharifa polisi?" Trigger aliuliza,



"huyu ni wa kumalizwa" Harry aliongea,



"ndio maana siku ile nikawaambia tummalize, nyie mkakataa, sasa anakuja kututia presha" Trigger aliongea kwa kulalamika,



"wewe angalia usalama jengo zima, ili tujue namna ya kummaliza, kesho ikiwezekana" Harry aliongea,



"sawa, hii ni mbaya, mbaya sana" Trigger aliongea huku akiondoka kwenda kuangalia usalama ili wajue namna ya kummaliza Dokta Pendo siku inayofuata.



*****************



Siku iliyofuata, Sarah alikuwa bize sana na masuala ya kampuni yake, kwa hiyo hakuweza kwenda kabisa hospitali Nyakati za mchana ila alijitahidi sana kuwasiliana na muuguzi ili kujua maendeleo ya Dokta Pendo.



Ilivyofika jioni, Sarah aliamua kwenda hospitali, hakwenda na gari lake kwa ajili ya usalama, alikwenda na gari ndogo ya ofisi.



Sarah alivyofika hospitali alielekea moja kwa moja kwenye wodi aliyolazwa Dokta Pendo, ila kabla hajafika aliweza kumuona mtu aliyemtia mashaka, alikuwa ni Trigger, tena alikuwa akiranda randa kwenye eneo la ile wodi, hakuweza kuingia kwa kuwa ndani ya ile wodi walikuwepo watu waliokwenda kumtazama Dokta Pendo.



Sarah akasubiri kwa muda mpaka Trigger alipopotea eneo lile, kisha kwa hatua za haraka akaenda kuingia ndani ya wodi, wakati Sarah akiingia na watu waliokuwa ndani walikuwa wanamuaga Dokta Pendo, kwa maana hiyo walikuwa wanaondoka. Watu walivyoondoka, Sarah akamsogelea Dokta Pendo,



"kuna hatari tuondoke" Sarah aliongea kwa sauti ya chini,



"hatari gani?" Dokta Pendo aliuliza,



"wale waliokuteka nimewaona wakiranda nje ya wodi hii" Sarah aliongea,



"acha waniue tu" Dokta Pendo alijibu kijeuri,



"acha ujinga wewe, mimi nakubeba tunaondoka" Sarah aliongea kwa jazba,



"Sarah nilishakuonya Kaa mbali na mimi, usinizidishie matatizo, haya uliyonipa yananitosha, na kama utalazimisha unitoroshe hapa, nitapiga kelele za kuomba msaada" Dokta Pendo aliongea,



"siwezi kukuacha wakuue" Sarah aliongea na kumpiga ngumi ya kisogo Dokta Pendo, Dokta Pendo akapoteza fahamu, Sarah akamuweka kwenye kiti cha matairi na kuanza kumsukuma kuelekea nje.



Sarah alivyotoka tu ndani ya wodi, ndio muda huo Trigger akaingia na bastola mkononi, lakini cha ajabu hajakuta mtu, akahisi kuchanganyikiwa, akatoka mbio na bastola mkononi, akapishana na daktari, daktari akaogopa baada ya kuiona bastola, lakini Trigger hakumdhuru, alimpita tu.



Daktari akahisi hatari, ndipo kuanza kukagua wodi na akakuta wodi moja haina mgonjwa, daktari akahisi mgonjwa ametoroshwa, akakimbilia alarm na kobonyeza, baada ya dakika mbili polisi walijaa eneo la hospital, daktari akawaeleza kila kitu, polisi wakazunguka hospitali nzima, hakuna gari kutoka bila kukaguliwa, na kumbuka Sarah alikuwa bado gari yake ipo ndani ya uzio wa hospitali, alishangazwa na hali ya polisi kujaa eneo lile, akapata hofu huku akihisi huenda imegundulika mgonjwa ameibwa au kuna tukio jingine lisilo la kawaida limetokea.



Sasa Sarah akataka kuwasha gari na kuliondoa kwa kasi, ila alipata mashaka kutokana na gari aliyokuwa nayo leo, haikuwa na kasi kama range Rover yake.



wakati gari yake ikiunguruma huku akiwaza cha kufanya, na muda huo Dokta Pendo alikuwa anazinduka,



"Sarah nirudishe wodini, napiga kelele" Dokta Pendo aliongea huku machozi yakimtoka, alikuwa amekalishwa siti ya nyuma, ila kabla Sarah hajasema kitu, mlango wa gari yake ulifunguliwa ghafla, akashtuka, na kumtazama mtu aliyefungua, alikuwa ni polisi, na tena nyuma ya huyo polisi walisimama polisi wengine wawili,



"shuka chini" Polisi aliongea huku akimmulika Sarah usoni kwa kutumia tochi, Sarah akachoka kabisa na wakati huo sura ya dokta Pendo ilichanua kwa tabasamu..................









"kuna nini kwani" Dokta Pendo aliuliza huku akitabasamu,



"kumbe mpo wawili? Shukeni chini" Askari aliongea kwa ukali,



"kuna nini kwani? Mbona unaongea kwa ukali hivyo? Sema shida acha kupayuka" Dokta Pendo aliongea kwa ukali huku Sarah akiwa ameegemea staring ya gari yake,



"samahani dada, kuna mgonjwa ameibiwa ndani, kwa hiyo hapa tunakagua magari tukimtafuta huyo mgonjwa" Askari mwingine aliongea huku akimsogeza yule askari wa mbele aliyekuwa anaongea kwa ukali,



"sawa, wewe nimekuelewa, nyie kagueni tu, mimi siwezi kushuka kwa maana nimetoka kufungwa bandeji ngumu miguuni sasa hivi, nyie kagueni tu" Dokta Pendo aliongea na kumfanya Sarah astahajabu, hakudhani wala hakufikiria kama Dokta Pendo angeongea maneno yale,



"sawa. Kagueni mpaka kwenye buti" Askari aliongea huku akiwageukia wenzake ambao walianza ukaguzi na kipindi hicho chote Sarah alikuwa amelalia staring huku akifikiria namna Dokta Pendo alivyomtetea.



"mnaweza kwenda sasa" Askari aliongea huku akimshika kichwa Sarah, Sarah akanyanyua kichwa huku hataki kuongea, yaani alishindwa aongee nini. Sarah akaanza kuiondoa gari huku akiangalia mlango wa lile jengo la hospitali, akawaona Trigger na Harry wakitoka,



"angalia kule" Sarah aliongea huku akiwanyooshea kidole na kufanya Dokta Pendo atupe jicho, aliwaona ila hakuongea kitu, machozi yalikuwa yakitiririka tu huku akiamini Sarah ameletwa duniani kumuharibia maisha.



Sarah baada ya kuona Dokta Pendo yupo kimya na analia, akaamua akae kimya na kuendelea kuendesha gari kwa mwendo wa wastani, alikuwa anaelekea kwake.



Iliwachukua takribani dakika kumi na tano na kufika nyumbani kwa Sarah, Sarah akaingiza gari ndani ya geti na kisha akashuka na kutembea kwenye chumba chake cha siri na kuchukua kiti cha matairi na kurudi nacho nje, kisha akamshusha Dokta Pendo na kumpeleka moja kwa moja kwenye chumba chake cha kawaida ambacho hutumiaga yeye.



Alipomfikisha akimuweka kitandani, kisha akaelekea tena kwenye chumba chake cha siri na kurudi na vyuma ambavyo alitumia kutundikia miguu ya Dokta Pendo na kufanya awe kama amelazwa hospitali.



"Pendo usinichukulie tofauti, mimi nimefanya yote haya kwa ajili yako" Sarah aliongea huku akikaa jirani na dokta Pendo, lakini Dokta Pendo hakutaka kuongea, aliendelea tu kulia, Sarah akaona asimsumbue zaidi, akaamua aende sebuleni kuangalia runinga, hakutaka kuongea na Dokta Pendo akiwa kwenye hali ile, aliamini kabisa Dokta Pendo ana msongo wa mawazo.



****,***********



Trigger baada ya kusikia kengele ya hatari imepigwa pale hospitali, alimkimbilia moja kwa moja kwenye wodi aliyolazwa Taita na kumkuta Vin na Harry wakiwa wamesimama nje ya wodi,



"kuna nini uko, mbona wamepiga kengele ya hatari?" Vin alimuuliza Trigger,



"hata sijui, huenda kuna itilafu" Trigger alijibu na wakati huo huo kuna daktari aliingia pale,



"samahanini waungwana, hatakiwi mtu Kuwa ndani ya wodi. Kuna tatizo limetokea" Daktari aliongea huku akiwa amesimama mbele yao,



"tatizo gani Dokta?" Vin aliuliza,



"Kuna watu wameingia na silaha na wamemuiba mgonjwa" Daktari alijibu,



"usalama hakuna kabisa hapa, mtu anawezaje kuingia ndani ya wodi na kumuiba mgonjwa?" Harry aliuliza kwa hasira,



"ni tukio la ghafla boss, tunawaomba mtoke tu nje, maelezo mengine mtayapata uko nje" Daktari aliongea kistaharabu wakati wakiwa Vin wakitoka,



"mgonjwa wa wodi namba ngapi ameibiwa?" Yule mama Muuguzi alimuuliza daktari,



"namba tano" Daktari alijibu,



"Dokta Pendo!!!?! Dokta Pendo ndio amechukuliwa?" Mama Muuguzi aliuliza huku akishangaa na sauti yake iliweza kupenya vyema masikioni kwa Trigger na Harry, wakaangaliana na kisha wakaendelea kutembea.



Walienda mpaka nje, wakaingia ndani ya gari Vin na Trigger, na Harry nae akaingia kwenye gari nyingine na kisha safari ya kurudi Vin hotel ikaanza.



Walipofika Vin hotel, Vin alitelemka na kuwaaga wenzake kwa minajili ya kukutana siku inayofuata asubuhi ili waende hospitali. Baada ya maagano hayo Vin aliingia zake ndani ya hotel.



Trigger akatoka ndani ya gari lake na kwenda kuingia kwenye gari la Harry,



"ni Sarah atakuwa amemtorosha Dokta Pendo" Trigger aliongea huku akiwasha sigara,



"kama ni Sarah amemtorosha, basi inawezekana kabisa Sarah amejua kuwa sisi uwa tunaenda hospitali" Harry aliongea huku akishusha kioo cha gari baada kukereka na moshn wa sigara aliyokuwa akivuta Trigger,



"sasa kama nilivyokueleza hawali, tuna hatari sana, maana Dokta Pendo anajua kambi yetu ilipo, anaweza kumuelekeza Sarah" Trigger aliongea,



"sasa tunafanyaje? Mimi nadhani tumuondoe babu yake Sarah, tumuhamishie sehemu nyingine" Harry alitoa ushauri,



"hapana, cha muhimu ni kuongeza ulinzi, tena nitaongeza vijana wengi walizunguke eneo la kambi" Trigger aliongea kisha akapuliza moshi wa sigara,



"nalo ni jambo zuri, je unavyodhani huu ni muda sahihi wa kumshirikisha Vin katika mpango huu?" Harry aliuliza,



"tungoje mzee wake aamke, maana tunaweza kumwambia sisi kumbe Taita hakupanga kumwambia" Trigger aliongea,



"sawa, basi nadhani tuachane, tutakutana hiyo kesho asubuhi" Harry aliongea,



"poa" Trigger aliongea huku akitelemka katika gari na kumuacha Harry akiondoka taratibu na gari yake, Trigger akaifuata gari yake na kuingia, kisha akapeleka mkono siti ya nyuma na kuchukua chupa to pombe kali, akaigida huku amekuja uso, baada ya hapo akawasha gari na kuiondoa kwa mwendo wa kasi.



*****************



Sajenti Minja alifika hospitali na kukutana na ulinzi mkali, akafanikiwa kufika mpaka katika mlango wa jengo la hospitali na kuizuiliwa kuingia,



"kuna nini kwani?" Sajenti Minja aliuliza,



Kuna tatizo limetokea ndani" Askari aliyekuwepo mlangoni aliongea,



"tatizo la kiusalama au la kiufupi?" Sajenti Minja alihoji,



"Kaka nimeshakujibu, maswali mengine ya nini? Wewe unauliza kama nani?" Askari aliongea kwa ukali,



"naitwa Sajenti Minja" Sajenti Minja aliongea huku akimuonesha kitambulisho yule askari, askari akapoa baada ya kugundua ni mkubwa wake huyo,



"kuna mgonjwa ameibiwa mkuu, yaani amechukuliwa na watu wenye silaha" Askari alitoa maelezo,



"nipishe nipite sasa" Sajenti Minja aliongea na kisha yule askari akaachia njia, Sajenti Minja akawa anaelekea kwenye wodi aliyolazwa Dokta Pendo, ila kabla hajaifikia alikutana na yule mama mtu mzima ambaye ni muuguzi,



"Baba, Dokta Pendo amechukuliwa na watu wasiojulikana" Muuguzi alitoa taharifa iliyomtetemesha Sajenti Minja,



"muda gani?" Sajenti Minja aliuliza kwa sauti iliyoonesha haina nguvu,



"nusu saa iliyopita ndio tumegundua jambo hilo" Muuguzi alijibu kwa upole,



"kwa hiyo hospitali imefanya jambo gani baada ya kugundua hilo tukio? " Sajenti Minja aliuliza,



"sijui kitengo cha usalama wameamua kufanya jambo gani?" Muuguzi alijibu kinyonge,



"sawa mama, ngoja nikawaulize" Sajenti Minja aliongea huku akigeuza na kuanza kuondoka kuelekea nje ya jengo, tayari akili zake zilivurugika kutokana na taharifa ile, Sajenti Minja akatoa simu na kumpigia Dokta Pendo, simu iliita mpaka ikakatika, akarudia tena na tena lakini hali ikawa vile vile, mwisho simu ikawa hazipatikani hewani, Sajenti Minja akakunja sura kwa hasira, akaanza kuelekea kwenye gari lake, alivyofika akaingia na kujishika kichwa, mawazo yalimtawala, akachukua simu yake na kumpigia Sarah,



"upo wapi?" Sajenti Minja aliuliza baada ya simu kupokelewa,



"ndo natoka kazini" Sarah alidanganya,



"umesikia Dokta Pendo ametekwa tena hospitalini Leo?" Sajenti Minja aliuliza,



"unasemaje?, acha kunitia presha" Sarah aliongea huku alijifanya ameshtuka,



"kweli, nipo hospitali hapa ndio nikekutana na hizo habari" Sajenti Minja aliongea,



"jamani mbona wazembe hivyo hapo hospitali? Sasa inakuaje?" Sarah aliuliza huku akijifanya amechanganyikiwa kabisa,



"sijui, kapumzike kwanza, nitakutafuta kesho" Sajenti Minja aliongea,



"ni kweli ametekwa au unanitania?" Sarah aliuliza tena ,



"kapumzike, tutaongea kesho" Sajenti Minja aliongea na kukata simu.



Sarah nae baada ya Sajenti kukata simu, Sarah akaitupia simu mezani na kisha akaichukua simu ya Dokta Pendo, alikuwa nayo yeye, baada ya kuichukua akaitoa betri kabisa, na kuiweka kwenye droo ya kabati.



*****************



Siku mpya ilianza, siku hiyo Sarah aliamua kushinda nyumbani ili awe karibu na Dokta Pendo, alimpa huduma zote muhimu, alijitahidi kuongea nae, lakini Dokta Pendo hakuwa akitamani kumuona hata Sarah,



"najua ni ngumu kunielewa kwa sasa, ila baadae utanielewa tu" Sarah aliongea huku akimlisha Dokta Pendo,



"hutaki kuongea, ila naomba unisaidie kitu, tokea wamemteka babu yangu sijawahi hata kumuona, yaani sijui ni mzima au amekufa?" Sarah aliongea huku machozi yakimtoka,



"na huyo ndio mzazi wangu na ndugu yangu pekee, bila huyo duniani mimi si kitu tena, sina baba wala sina mama, ni yeye ndio mtu ninaepata faraja kutoka kwake" Sarah aliongea kisha akatoa kitambaa na kujifuta machozi, Dokta Pendo roho ya huruma ikamuingia,



"nitakuelekeza kambi yao ilipo, ila niahidi hutokwenda peke yako, utaenda na polisi" Dokta Pendo aliongea huku akiwa hataki kumuangalia Sarah,



"sawa, nitaenda na polisi" Sarah alijibu huku akiwa ahamini kama Dokta Pendo ametamka maneno hayo.



Baada ya hapo Dokta Pendo akamuelekeza kila kitu sehemu ilipo kambi ya Taita.



"nashukuru sana shoga yangu" Sarah aliongea huku akimkumbatia lakini Dokta Pendo hakuongea tena.



Ilipofika mida ya saa mbili usiku, Sarah alikuwa ameshaandaa chakula na kumlisha Dokta Pendo, kisha yeye akawa amekaa jirani na dokta Pendo, ilipofika saa tatu na nusu Dokta Pendo alikuwa amekwishalala, Sarah akaenda sebuleni na kuangalia runinga.



Ilipofika saa tano usiku, Sarah aliingia kwenye chumba chake cha siri na kuingia kujiandaa, alivaa kikazi kwa maana alipanga kwenda kuvamia kambi ya Taita.



Sarah alimalza kujiandaa na kutoka na gari yake, ramani yote ya kufika kwenye nyumba ambayo ni kambi ya Taita ilikuwa kichwani.



Sarah aliacha gari yake mtaa wa pili na kisha akatembea kwa miguu na kuweza kufika kwenye hiyo nyumba ambayo ilikuwa na uzio mrefu sana, Sarah akapanda kwenye mti uliokuwa jirani na ukuta, kisha akaweza kuyaona mazingira ya ndani vizuri, Sarah aliwaona vijana wawili tu ndani ya uzio, Sarah akaruka na kutua ndani, wale vijana wakashtuka na kutaka kuchomoa silaha, Sarah akawarushia visu vilivyopenya katika shingo zao. Sarah akafanikiwa kupenya ndani, cha ajabu hakukuta upinzani ambao aliutegemea, yaani hakukuta mtu hata mmoja.



Sarah akawa anatembea kwa uangalifu huku akijitahidi kufungua kila chumba ili aweze kumuona babu yake, lakini hakufanikiwa.



Akiwa amekata tamaa kabisa, Sarah alifungua chumba cha mwisho, alikuta kipo giza ila alihisi kuna mtu anahema kwa nguvu sana, Sarah akapapasa ukutani ili atafute switch ya taa, hakuiona, akaamua kufuata sauti ya mihemo inapotokea, ghafla akamulikwa usoni na tochi yenye mwanga mkali, kisha taa ya chumba kile ikawashwa, alishangaa kumkuta Trigger juu ya kile kiti, yeye ndio aliutengeneza mtego ule wa kumnasa Sarah,



"karibu himayani malaya mtoto" Trigger aliongea huku amekamata bastola yake mkononi, Sarah akataka kurudi mlangoni ili akimbie, ghafla mlangoni akatokea Harry huku nyuma yake akiwa Tekso na Strategic na wote walikuwa na silaha nzito za kivita,



"jisalimishe" Harry aliongea huku akisimama na pia akitoa tabasamu la ushindi. Sarah akazungusha macho kama mtu anayefanya tathmini, ila aliona hawezi kufua dafu mbele ya wanaume wale wenye silaha nzito, Sarah akatoa silaha zake zote na kuzitupa chini, akapiga magoti na Mikono akaiweka juu, Sarah alisalimu amri ingawa hukupenda, aliamua akubaliane na matokeo bila kujua kuwa huenda mwisho wake umekaribia....................







"mfunge kamba malaya huyu" Harry aliongea kisha Trigger akanyanyuka na kuchukua kamba na kumsogelea Sarah,



"weka mikono nyuma malaya wewe" Trigger aliongea huku akiivuta mikono ya Sarah kwa nyuma, kisha akamfunga kamba mikononi na kisha akamsukuma kwa mbele, Sarah akaangukia tumbo, kisha Trigger akaishika miguu ya Sarah na kuifunga kwa kamba, sasa rasmi Sarah akawa mateka wa vijana wa Taita.



"katundikeni kwenye chumba cha mateso" Harry aliamrisha kisha Trigger na Tekso wakamkamata Sarah mkono wa kushoto na Tekso alikuwa upande wa kulia wa Sarah , wakaanza kumpeleka, walifika sehemu katika eneo la sebuleni na kuondoa meza, kisha wakakuta kuna mfuniko kama wa chemba, wakauvuta na kumfanya kuuweka pembeni, kisha wakaingia kwa kutumia ngazi wakaanza kushuka chini, muda wote Sarah alikuwa akishangaa namna hiyo sehemu ilivyojificha.



Walipofika chini walikuta korido ndefu, wakaanza kuifuata mpaka katika mlango mmoja uliokuwa na kufuri nzito, Trigger akatoa funguo na kufungua ile kufuri, kisha wakamuingiza Sarah ndani, Kisha wakamfunga katikati ya chumba ambapo sehemu ya juu kulikuwa na vyuma vinaning'inia, wakaifunga mikono ya Sarah juu katika vile vyuma na miguu yake ikabaki ikining'inia, yaani haikufika chini,



"sasa leo nataka unijibu maswali yangu machache" Harry aliongea huku akivuta kiti na kukaa, ila Sarah hakuonesha kuogopa, alitabasamu tu,



"kwanini unataka kutuua?" Harry aliuliza,



"kuwaua? Kama ningetaka kuwaua basi wewe ningeshakuua zamani, bado sijataka kuwaua, bado nangoja nyie mtake kufa wenyewe" Sarah alijibu huku akitabasamu,



"lini sasa wakati wewe hapo ulipo ndio mwisho wako" Trigger aliongea kwa kejeli huku akicheka,



"hakuna anaejua mwisho wangu, na wala huu hautakuwa mwisho wangu" Sarah alijibu kijeuri,



"mpumbavu wewe upo kwetu bado unatujibu jeuri?" Trigger aliongea huku akimrushia Sarah ngumi kali iliyotua kwenye mdomo wa Sarah na kumfanya Sarah ageuze shingo na kutema damu,



"nadhani wewe ni mzuri sana kwenye matumizi ya silaha, ila kwenye matumizi ya ngumi hauna kitu, nimelithibitisha hilo, ngumi yako ni nyepesi sana, kama ya binti wa miaka kumi na mitano" Sarah aliongea huku akitoa kicheko kikubwa cha dharau,



"mpuuzi wewe, leo nitakuua, nitakuua kwa mkono wangu" Trigger aliongea na kumrushia Sarah ngumi mbili zilizomfikia usoni na nyingine ikatua kwenye pua ya Sarah, damu ikawa inamchuruzika Sarah kwenye pua yake,



"hizo ngumi zote zingekuwa ni za mwanaume aliyekamilika, nadhani ningekuwa nimepoteza fahamu au ningekuwa nimeshakufa" Sarah aliongea, ila safari hii hakua akicheka tena, alikuwa akisikitika huku akimuangalia kwa jicho la dharau,



"malaya wewe nitakuua" Trigger aliongea kwa hasira huku akijiandaa kurusha ngumi nyingine,



"tulia wewe, huyo anakupa wendawazimu tu, usiangaike kupambana nae, tutakuwa nae muda wote hapa, utampiga utakavyo na utamtafanya utakavyo, hata mkiamua kumbaka kwa zamu mnaweza" Harry aliongea huku akiwa ameushika mkono wa Trigger na kumuacha,



"Harry una akili sana, nadhani wazazi wako waliona mbali na ndio maana wakaweka dhamira mpaka ukafika chuo kikuu na ukabobea kwenye masuala ya sheria, ila ulichobobea haukitendei haki, unaonea wanyonge kwa sababu ya fedha, umegeuzwa mbwa wa mwenye fedha, unatumiwa kinyume na matarajio ya ulichokisomea, umekuwa mtumwa" Sarah aliongea huku akimtazama Harry,



"binti kuna kitu umsaahau, wazazi wangu walinisomesha kwa juhudi na bidii ili nije kuwa na fedha na niwasahidie kipindi wakizeeka, hicho ndicho ninachokifanya, nipo kwa ajili ya kupata pesa, hujakosea kusema ninatumikishwa kwa ajili ya pesa" Harry alijibu kwa umakini huku akiwa amemkazia macho Sarah,



"unatumikishwa kwa pesa, ila siku ya kifo chako itaandikwa umekufa kwa ajili ya haki" Sarah aliongea huku akitabasamu,



"sasa binti sio kila jambo jema nililolifanya napaswa kulitangaza, kuna mambo mema mengi sana nimeyafanya katika upande wa haki, so usinihukumu kwa kuwa sijawahi kufanya jema mbele yako" Harry aliongea huku nae pia akitabasamu,



"je unaweza kunisaidia kitu ili nikuhesabu kuwa ni mmoja kati ya watu wema niliowahi kukutana nao?" Sarah aliuliza,



"nikusaidie nini?" Harry aliuliza,



"naomba uwe shahidi au uwe mwanasheria wangu katika kesi nitakayoifungua dhidi ya vifo vya wazazi wangu" Sarah aliongea huku akimuangalia Harry,



"utafungua lini sasa wakati huu ndio mwisho wako?" Trigger aliuliza kwa dharau huku akicheka,



"wewe huwezi ujua mwisho wangu kama mwanzo wangu hukuwahi kuujua" Sarah alijibu kwa sauti ya utulivu,



.



"kama ukiweza kutoka hapo, nitakusaidia" Harry alijibu huku akinyanyuka na kuondoka zake, aliamini kabisa Sarah hana ujanja tena wa kutoka pale alipo, na pia aliamini katika ule mchakato wake wa kumuua Sarah ili abakie na amani.



Huku ndani Trigger aliendelea kutamba mbele ya Sarah,



"Mimi usiku nitakupiga tu mpaka nichoke, sina sababu ya kukupiga, nakupiga kufurahisha nafsi" Trigger aliongea huku akiokota mnyonyoro uliokuwa unazagaa sakafuni,



"ukiamua kunipiga, nipige mpaka nife, ukiniacha hai ama ukanivunja kila kiungo changu ila ukaniacha nikipumua, huo utakuwa muendelezo wa makosa yako dhidi yangu, kama tutakutana tena, ndio itakuwa tamati yetu, mmoja lazima afe" Sarah aliongea kwa kujiamini,



"wewe maliza maneno yote, mimi siongei tena, leo nakupiga tu, kesho ndio nitakuuliza maswali" Trigger aliongea kisha akawaruhusu Tekso na Strategic waondoke, akabaki yeye na Sarah, Trigger akamuondoa fulana Sarah na kumuacha mgongo wazi, akaanza kumtandika kwa kutumia ule mnyonyoro, alimtandika sana, Sarah alilia mpaka sauti ikamkauka, mwisho akalegea, macho yakajaa giza na baada ya hapo ubongo haukuwa na mawasiliano tena na dunia, Sarah alilegeza shingo na kufunga macho, lakini Trigger aliendelea kumpiga tu, mpaka aliporidhika, akazima taa ya kile chumba na Kutoka zake kifua mbele, leo alimkamata mwizi wake baada ya arobaini nyingi zisizo na idadi.



***************.



Asubuhi ya leo Sajenti Minja aliamkia hospitali, wakati yupo njiani akielekea hospitali, njiani habari ilikuwa ni kuibwa mgonjwa katika hospitali kubwa na yenye hadhi, magazeti yote na radio zilikuwa ni habari hizo hizo na kila mtu mtaani alikuwa anaongea lake, wapo waliolaani hicho kitendo na wapo pia walituhumu uzembe wa watu wa usalama wa hospitali na wapo wengine waliomlaumu mgonjwa.



Njia nzima Sajenti Minja mawazo yake yalikuwa ni kuwaza hilo tukio, huku akijaribu kutengeneza picha namna hao watu wakiingia hospitali na kufanya uharifu huo.



Sajenti Minja akafika eneo la hospital na kuomba kuonana na mkurugenzi wa hospitali, akaruhusiwa,



"kama nilivyojitambulisha hapo hawali, mimi ni askari na huyo mgonjwa aliyechukuliwa alikuwa na kesi ambayo nilikuwa naipeleleza mimi, kwa hiyo basi, ningependa kuona camera za matukio yote ya jana usiku" Sajenti Minja alizungumza kwa utulivu,



"hakuna shida mkuu, twende chumba cha usalama" Mkurugenzi wa hospitali aliongea huku akisimama na kutangulia kutoka nje huku Sajenti Minja akimfuata kwa nyuma. Safari yao iliishia kwenye mlango mmoja ulioandikwa "security room", mkurugenzi akagonga mlango na ukafunguliwa na kijana mmoja aliyevaa sare za rangi ya blue tupu na kiatu cheusi,



"karibu mkurugenzi" kijana aliongea huku akiwa amesimama mlangoni,



"huyu ni askari mpelelezi, ana kitu anataka kuangalia kwenye record za jana" Mkurugenzi aliongea,



"karibu, pita ndani" Kijana aliongea huku akiacha njia Sajenti Minja apite,



"sasa mimi acha nikuache, nimekufikisha sehemu husika" Mkurugenzi aliongea huku akimpa mkono Sajenti Minja,



"shukran mkurugenzi, nitakuona nikitoka hapa" Sajenti Minja aliongea huku akitabasamu, kisha akaingia ndani na kuoneshwa sehemu ya kukaa, alikaa pembeni ya yule kijana,



"jana usiku ulikuwepo?" Sajenti Minja alimuuliza yule kijana,



"nilikuwepo toka jana mchana" kijana alijibu,



"ok, ebu weka camera ya wodi namba tano kisha uirudishe mpaka Nyakati za jana usiku wakati wa tukio" Sajenti Minja alimwambia yule kijana, yule kijana akairudisha ile camera mpaka muda huo, lakini walionekana wale wageni wa hawali tu waliongia kumuona Dokta Pendo, baada ya hapo camera zikakata mawasiliano,



"huyu aliefanya hili tukio huenda ni mtaalam sana au anayajua mazingira yote ya hapa" Sajenti Minja aliongea huku akisikitika,



"na hata nilipoangalia camera za nje pia sikumuona, nazo zilikuwa zinakata kama hivyo" Kijana aliongea huku akimuwekea Sajenti Minja nae ajionee,



"nashukuru mista, nitarudi tena endapo kutakuwa na ulazima wa kufanya hivyo" Sajenti Minja aliongea huku akisimama na Kuondoka zake, aliweza kupishana na baadhi ya waandishi wa habari wakiwa wapo bize kuhoji wafanyakazi wa hospitali ile.



Sajenti Minja alienda mpaka kwenye gari lake na kuingia, kisha akatoa simu na kumpigia Sarah, simu haikuita, akajaribu tena kupiga namba za Dokta Pendo, pia simu haikuwa hewani, Sajenti Minja akaenda zake ofisini kuendelea na kazi zake.



************************



Dokta Pendo alifungua macho saa mbili asubuhi, hakumkuta Sarah pembeni yake, akadhani huenda yupo jikoni anapika.



Saa tatu asubuhi ikafika lakini hakuona dalili zozote za Sarah kuwepo, akahisi huenda ameenda sokoni.



Saa nne ilipofika hakuona uwepo wa Sarah, Dokta Pendo akajiuliza hata kama sokoni, hilo soko lipo umbali gani? Dokta Pendo akatoa mawazo ya Sarah kuwepo sokoni, akaweka mawazo huenda Sarah ameenda kazini na labda atarudi mchana, akawaza sasa kwanini amshindishe na njaa?



"huyu mwanamke alaaniwe, kwanini anitese hivi??? Si bora angeniacha hospitali?" Dokta Pendo aliongea peke yake huku njaa ikimtafuna, tena kwa kwa kasi ya ajabu.



Mwishowe ikafika saa kumi, Dokta Pendo akaanza kutukana matusi yote makubwa kumuelekea Sarah, kibaya zaidi Dokta Pendo alianza kunyong'onyea kutokana na njaa na pia alikuwa amemeza dawa kali zilizopo kwenye droo ya kitanda pembeni yake. Njaa iliendelea kumuuma na kunyanyuka alikuwa hawezi, akaanza kupiga kelele ili hata mtu akipita amsikie, lakini haikuwezekana kwa sababu nyumba ya Sarah ilijitenga sana, akaamua anywe maji yote yaliyokuwa kwenye chupa pembeni yake.



Saa mbili usiku ikamkuta Dokta Pendo yupo Hoi kitandani, taabani, alichokuwa anakifanya ni kumuomba Mungu huku akilaani kitendo hicho anachofanyiwa na Sarah, kitu ambacho hakukijua ni kuwa muda huo Sarah alikuwa kwenye hali hatari zaidi yake, japo Sarah alikuwa kwenye hatari na akiwa katika hali mbaya kiafya, bado alimuomba Mungu amsaidie Dokta Pendo jambo lolote baya lisimpate.



*****************



Wakati Sarah na dokta Pendo wakiwa katika hali hizo tete, Sajenti Minja mawazo yalikuwa yameaongezeka zaidi baada ya kufokewa na mkuu wake kama mtoto mdogo, alionekana ni mzembe aliyeshindwa kuifanya kazi yake kwa weledi.



Mida hii ya saa tatu usiku, Sajenti Minja alikuwa anajiona ni mtu mwenye hatia sana, aliona jambo lolote baya litalomkuta Dokta Pendo, basi yeye atahusika kwa namna moja au nyingine hata kama hatokuwa mlengwa wa moja kwa moja.



Na muda huu wa saa tatu usiku, Sajenti Minja alikuwa akielekea nyumbani kwa Sarah baada ya kupata wasiwasi kwa maana tokea asubuhi alikuwa akipiga simu na haikuita, na muda huu simu ya Sarah ikawa haipatikani kabisa, Sajenti Minja alikuwa hayupo kwenye hali nzuri kimawazo, kwanza alipanga kumfanya vibaya mtu yoyote atakayehisiwa na kupatikana na hatia juu ya matatizo ya Dokta Pendo.



Saa tatu unusu Sajenti Minja alikuwa anasimamisha gari yake nje ya nyumba ya Sarah, alikuta geti limefungwa, akataka kuondoka ila roho yake ikakataa, akapiga hesabu na kuamua aingie kwa njia isiyo sahihi, akaruka ukuta na kuingia ndani ya uzio wa nyumba, akaelekea kwenye mlango wa sebuleni, akajaribu kuusukuma mlango ukafunguka, akahisi hatari zaidi, akaingia kwa hatua za kunyata, akakuta sebuleni kuko giza, akawasha taa.



Dokta Pendo akiwa chumbani alisikia mtu akiwasha taa, akashukuru Mungu huku akiamini Sarah amerudi, akapanga kumnunia, tena mnuno wa kimataifa.



Sebuleni Sajenti Minja akakuta vitu vyote vipo kwenye utaratibu mzuri, akafungua droo na kuikuta simu ya Sarah,



"atakuwa ameenda kazini amemsahau simu" Sajenti Minja aliongea kwa sauti ya kawaida huku akiifunga droo, akazungusha macho kushoto na kulia, akazima taa akawa anaelekea mlango wa kumtoa sebuleni.



Dokta Pendo aliweza kusikia yote hayo, aliweza kuisikia mpaka sauti ya Sajenti Minja akaitambua, akaona huo ndio wakati wake wa kuwa huru na kutoka mikononi kwa Sarah, aliamua kuwa muwazi kwa Sajenti Minja.



ila kilichomtisha Dokta Pendo ni kuhisi kama Sajenti Minja anataka kuondoka, Dokta Pendo akavuta pumzi ndefu na kupiga kelele kubwa za kutaka msaada................





http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Bahati mbaya kwa Dokta Pendo ni kwamba, nguvu hakuwa nazo, hata sauti haikutoka, akajaribu tena, bado sauti haikutoka, kilichoweza kutoka kwa muda huo ni machozi tu, Dokta Pendo alianza kuuamini ule msemo wa wahenga, "siku ya kufa nyani miti yote huteleza"



Dokta Pendo akajaribu kujivuta, lakini bado mwili ulikataa, nguvu haikuwepo kabisa, tena mbaya zaidi hata mkono tu kuunyanyua alishindwa.



Dokta Pendo akatabasamu, aliamua kukingojea kifo chake kwenye kitanda cha ugenini, hakuwa akiamini kuna msaada mwingine tena, alichokiamini ule ni mchezo, aliyemchezea vile ni Sarah, chuki yake dhidi ya Sarah ikaongezeka Maradufu, akaamua afunge macho na kusubiri kile alichokiita kifo, ndio aliamini ndio msaada uliobakia dhidi ya mateso anayokumbana nayo.



********************



ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog