Search This Blog

Sunday 22 May 2022

BARUA NDEFU KUTOKA BAGHDAD - 1

 







    IMEANDIKWA NA : NYEMO CHILONGANI



    *********************************************************************************



    Simulizi : Barua Ndefu Kutoka Baghdad

    Sehemu Ya Kwanza (1)

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    mwanadishi kutoka nchini Tanzania, Erick Justo akiwa amechaguliwa kuwa mwandishi bora wa habari kwa Bara la Afrika mwaka huo. Ukiachana na furaha za Watanzania hao, hata yeye mwenyewe alifurahia kwa kuona kwamba ndoto ambayo alijiwekea toka kipindi cha nyuma, kwa wakati huo ilikuwa imetimia.

    Uso wake ulikuwa na furaha, moyo wake ulikuwa umefanana na furaha ambayo alikuwa nayo wakati huo. Kila alipokuwa akihojiwa na waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali vya habari, Erick hakuificha furaha yake.

    Watu ambao walikuwa wamekusanyika katika Ukumbi wa Blue Pearl uliokuwepo Ubungo Jijini Dar es Salaam ndani ya Jengo la Ubungo Plaza bado walikuwa wakimpongeza mwandishi Erick ambaye alichukua tuzo hiyo iliyokuwa ikitetewa na Boniface Youssour, mwandishi wa habari kutoka nchini Ivory Coast.

    Kila alipokuwa akihojiwa na waandishi wa habari, ni watu watatu tu ndio ambao walikuwa wakisikika akiwazungumzia, wa kwanza alikuwa mama yake, Bi Magreth ambaye alifariki kwa ajali ya gari miama minne iliyopita, baba yake, mzee Justo ambaye aliuawa kwa kupigwa risasi kwa bahati mbaya na wa tatu alikuwa mkewe mpendwa, Christina ambaye alikuwa mjauzito.

    Machozi ya furaha yalikuwa yakimtoka, ushindi ambao alikuwa ameupata ulionekana kuwa mkubwa katika maisha yake. Waandishi wa habari wa Shirika la Habari la CNN ambao ndiyo walikuwa wameitoa zawadi hiyo wakaamua kuandaa kipindi maalumu cha kufanya na Erick, kipindi ambacho waliamini kingemfanya kuonekana duniani kote.

    “Siamini mke wangu... siamini mpenzi...” Erick alimwambia mkewe mara baada ya kufika nyumbani.

    “Amini mume wangu. Wewe ndiye mwandishi bora katika mwaka huu” Christina alimwambia mumewe kipenzi, Erick.

    Siku ziliendelea kukatika, Watanzania waliendelea kujivunia kwa kumpata mwandishi aliyeonekana kuwa bora katika kipindi hicho. Watu wengine wakaanza kufuatilia makala mbalimbali ambazo alikuwa akiziandika Erick katika magazeti ya sehemu alipokuwa akifanyia kazi.

    Kila mtu aliyezisoma makala zake alipigwa na mshangao. Hawakuweza kuamini kama kulikuwa na mwandishi ambaye alikuwa akiandika mambo mengi mazuri na ya kuvutia kama ilivyokuwa kwa Erick.

    Baada ya siku tatu kupita Erick akatumiwa tiketi na viza kwa ajili ya kusafiri kuelekea nchini Marekani. Huko alihitajika kwa ajili ya kufanya mahojiano na mtangazaji maarufu duniani, Larry King wa Kituo cha CNN. Erick hakukuamini kama alitarajiwa kusafiri kuelekea nchini Marekani ndani ya siku chache zijazo.

    Kila kitu kilichokuwa kikitokea katika maisha yake kwa wakati huo kilikonekana kuwa kama ndoto ambapo baada ya muda fulani angeshtuka kutoka usingizini na kujikuta kitandani akiwa na mkewe. Kila wakati macho yake yalikuwa yakiangalia saa yake, dakika zilionekana kwenda taratibu sana tofauti na siku nyingine.

    Alitamani muda uende harakaharaka ili asafiri na kuelekea nchini Marekani kwa ajili ya kufanyiwa mahojiano juu ya ushindi wake huo. Kila siku alikuwa akipokea pongezi mbalimbali kutoka kwa watu tofautitofauti huku wakiendelea kumtakia mafanikio katika maisha yake.

    Baada ya siku tatu kumalizika Erick akaanza safari ya kuelekea nchini Marekani. Kila kitu kilichokuwa kikiendelea katika maisha yake bado kilionekana kuwa kama ndoto, hakuamini kama siku moja ingetokea kwake na kusafiri kuelekea nchini Marekani, nchi ambayo alikuwa akiisikia tu au kuiona katika televisheni.

    Ndani ya ndege hakulala, kila wakati alionekana kuwa na mawazo tu. Aliifikiria sana nchi ya Marekani, kuanzia uzuri na hadi maendeleo yaliyokuwa yakipatikana nchini humo. Hakuamini kama katika kipindi hicho alikuwa akielekea katika jengo kubwa la habari la kimataifa la CNN lililokuwa katika jiji la Atalanta.

    Kwake, ilionekana kama ndoto. Jina la Larry King mara kwa mara lilikuwa likisomeka kichwani mwake. Hakuamini kama alikuwa akielekea kuhojiwa na mwandishi huyo ambaye alikuwa akiwahoji masupastaa wengi duniani.

    Ingawa mara kwa mara alikuwa macho lakini akajikuta akianza kulala mara baada ya ndege kuondoka katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Cairo nchini Misri. Ndege iliendelea na safari huku Erick akiwa amepitiwa na usingizi mzito.

    Alikuja kuamka saa mbili asubuhi mara baada ya ndege kuingia katika Uwanja wa Amstadam nchini Uholanzi ambako walitakiwa kubadilisha ndege ili kuendelea na safari ya kuelekea nchini Marekani.

    Erick akateremka kutoka katika ndege na kuanza kupiga hatua kuelekea katika vyumba vya kupumzikia. Baridi kali ambalo lilikuwa likipatikana katika nchi mbalimbali za Ulaya lilionekana kumpa tabu. Kila wakati alikuwa akitetemeka tu japokuwa alikuwa amevaa koti zito.

    Aliyapitisha macho yake katika majengo mbalimbali marefu na yaliyokuwa yakivutia, hakuamini kama majengo yale yalikuwa yakipatikana katika dunia moja iliyokuwa ikipatikana nchi ya Tanzania.

    Hali ya hewa ikaonekana kubadilika mara baada ya kuingia ndani ya jengo la uwanja wa ndege. Hali ya joto ikaanza kupatikana, hiyo ilitokana na viyoyozi ambavyo vilikuwa vinaendelea kutumika ndani ya jengo hilo.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Do I know you? (Hivi nakufahamu?)” Erick alishtushwa na sauti ya mwanaume mmoja ambaye alikuwa amekaa katika kiti cha pembeni ndani ya jego lile.

    Erick akageuza macho yake na kuanza kumwangalia mwanaume yule, alimwangalia kwa makini huku akijaribu kuvuta kumbukumbu kama alikuwa amekwishawahi kumuona sehemu fulani lakini jibu lilikuwa hapana.

    “I don’t know. I mean, I don’t know you (Sifahamu. Namaanisha sikufahamu)” alijibu Erick.

    “Are you a famous? Maybe a musician, footballer or someone else (Wewe ni maarufu? labda mwanamuziki, mchezaji mpira au mtu mwingine?)” Mwanaume yule aliendelea kumuuliza Erick.

    “No. I’m just a journalist (Hapana. Mimi ni mwandishi wa habari)” alijibu Erick.

    “Are you Erick Justo? The Best Journalist of Africa this year? ( Wewe ni Erick Justo? Mwandishi bora wa Afrika?)” Mwanaume yule aliendelea kuuliza.

    “Yes,” alijibu Erick.

    “I’m Brian Michael, a jouranalist from BBC (Mimi ni Brian Michael, mwandishi wa habari kutoka BBC)” Mwanaume yule alijitambulisha.

    Huo ndio ukawa mwanzo wa mazoea baina ya Erick na Brian. Wakaanza kuongea pamoja mpaka kufikia kipindi kuonekana kama walikuwa wamekutana siku nyingi zilizopita.

    Mara baada ya kupumzika kwa muda wa dakika thelathini, abiria wote wakatakiwa kuelekea katika ndege yao kwa ajili ya kuendelea na safari ya kuelekea nchini Marekani.

    Brian na Erick wakakaa katika viti vya pamoja huku wakiongea mambo mengi kuhusiana na uandishi pamoja na maisha kwa ujumla. Mazoea yao yakaongezeka zaidi, mpaka inafikia muda wa kulala, walionekana kuwa kama watu waliofahamiana kwa miaka mingi iliyopit *****

    Hakukuwa na mtu ambaye alijua kwamba walikuwa wamefika nchini Marekani mpaka pale sauti ya kike ilipoanza kusikika wakitakiwa kufunga mikanda yao. Ndege ikaanza kutua huku saa ya ukutani ndani ya ndege hiyo ikinyesha kuwa saa tisa usiku.

    Mara baada ya ndege kusimama, abiria wote wakaanza kuteremka. Erick alibaki akiangalia majengo makubwa yaliyokuwa yakivutia ambayo yalikuwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Atlanta. Baridi lilikuwa kali nchini Marekani tofauti na Uholanzi au Tanzania alipotoka.

    Abiria wote wakaanza kutembea na kuelekea nje ya jengo la uwanja ule. Kila kitu kilichokuwa kikionekana mbele yake kilikuwa kigeni. Erick alijisikia kumuuliza Brian mambo mengi kuhusu nchi hiyo, alisita kufanya hivyo kwani alijua fika kwamba Brian hakuwa mwenyeji sana nchini Marekani.

    ‘ERICK JUSTO’ Bango moja lililoshikwa na kijana mmoja lilisomeka vizuri machoni mwake.

    Erick akaanza kupiga hatua kumfuata kijana yule na mara baada ya salamu wote wawili wakaanza kuelekea nje ya jengo lile na kupanda ndani ya gari moja dogo na safari ya kuelekea hotelini kuanza.

    Jiji lilionekana kupendeza mno, majengo mengi makubwa na marefu yalikuwa yakionekana machoni mwake. Kila alipokuwa akiangalia mandhari ya jiji lile na alipokuwa akifananisha na mandhari ya jiji la Dar es Salaam, aliona kulikuwa na sababu nyingi zilizowafanya vijana wengi kuzamia nchini humo.

    Gari likasimama nje ya hoteli moja kubwa iliyoitwa Jupiter Hill. Mhudumu ambaye alikuwa akihusika katika hoteli ile, akalisogelea gari lile na kumfungulia Erick mlango. Akaanza kuelekea moja kwa moja mpaka mapokezi.

    Kila kitu kilionekana kuwa tayari, akapelekwa katika chumba ambacho alitakiwa kukaa. Wala haukuchukua muda mrefu, chakula kikaletwa, alipokula akaelekea bafuni kuoga.



    “Unafikiri ni kitu gani kimekufanya kuwa mwandishi bora barani Afrika?” Lilikuwa swali lililosikika vyema masikioni mwa Erick.

    Erick alibaki kimya kwa muda, alimwangalia Larry King, mtangazaji maarufu wa kituo cha habari cha CNN. Majibu mengi yakaanza kumiminika kichwani mwa Erick, hakujua atoe jibu gani kwani kila jibu ambalo alikuwa akilifikiria lilikuwa likistahili kutolewa.

    “Uandishi wangu. Mambo mengi ambayo ninayaandika katika makala zangu. Nafikiri na hata upangaji wangu ambao nauona kuwa tofauti na waandishi wengine” alijibu Erick.

    Larry King akatingisha kichwa chake juu na chini hali iliyoonyesha kwamba alikubaliana na jibu ambalo alilitoa Erick.

    Mahojiano yaliendelea zaidi na zaidi, Erick aliendelea kutoa majibu mengi na yaliyokuwa yakimvutia kila aliyekuwa akikiangalia kipindi kile kupitia televisheni ile. Erick alizidi kuonekana bora na kuzidi kukubalika kwa kila aliyekuwa akimsikiliza.

    Mara baada ya kipindi hicho kumalizika, moja kwa moja Erick akachukuliwa na kuanza kupitishwa katika sehemu mbalimbali ndani jengo la kituo hicho cha habari. Kila wakati Erick alikuwa akionekana kuwa na furaha, hakuamini kama angepata nafasi maishani mwake ya kutembelea kituo hicho cha habari.

    “Nimefurahi sana, ninajiona kutokumini kama leo hii niko ndani ya jengo hili kubwa la habari la CNN” Erick alimwambia mkurugenzi wa kituo hicho, Bwana Swan Godlove.

    Muda wa kula ulipofika, Erick akaitwa ndani ya chumba maalumu kwa ajili ya kupata chakula cha mchana. Ingawa chakula alicholetewa kilionekana kuwa kigeni lakini kilikuwa ni chakula kitamu ambacho hakuwahi kula hata siku moja.

    Erick hakutamani kurudi nchini Tanzania, siku tatu ambazo tayari alikuwa ameishi nchini Marekani zilionekana kubadilisha maisha yake na hata afya yake.

    “Utasafiri na kuelekea nchini Iraq” Mkurugenzi wa habari wa kituo hicho cha CNN, Bwana Swan alimwambia Erick.

    “Umesemaje?” Erick aliuliza kwa mshtuko.

    “Utasafiri na kuelekea nchini Iraq, huko utakwenda kuandika mambo mengi ambayo yanaendelea nchini humo, yaani katika hili namaanisha utakuwa mwakilishi wetu nchini humo kwa muda wa wiki tatu” Bwana Swan alimwambia.

    Furaha yote iliyokuwepo ndani ya moyo mwake ikatoweka, jina Iraq likaonekana kumtisha kupita kawaida. Kwa haraka sana kichwa chake kikaanza kurudisha matukio kadhaa ambayo yalikuwa yametokea nchini Iraq.

    Alivikumbuka vita ambavyo vilikuwa vikiendelea nchini humo, alimkumbuka hata mwandishi wa habari wa Kijapan ambaye alichinjwa mbele ya kamera na picha ile kuwekwa katika mitandao mingi ya Internet duniani.

    Kila alipokuwa akifikiria zaidi, Erick aliendelea kukosa amani kabisa. Mwisho wa maisha yake ukaonekana kukaribia. Safari ya kwenda nchini Iraq ikaonekana kuwa mwisho wa kila kitu maishani mwake.

    Hiyo ilimaanisha kuwa ndio ulikuwa mwisho wa kuvuta hewa ya dunia hii, hiyo ilimaanisha kuwa ndio mwisho wa kumuona mke wake mpendwa, Christina ambaye alikuwa mjauzito kwa wakati huo.

    Hakuamini kama angeweza kunusurika kutoka nchini Iraq salama. Safari hiyo ilimfanya kujiona kuishi kama mfu ambaye alikuwa akitembea. Tumaini la kuendelea kuishi likapotea moyoni mwake, alijiona kuwa tayari alikwishakufa.

    Hotelini hakulala vizuri, mambo mbalimbali ambayo alikuwa akiyaangalia katika televisheni, mambo ambayo yalikuwa yakitokea nchini Iraq bado yalikuwa yakiendelea kumtisha. Aliyakumbuka vizuri majambia ambayo Waarabu walikuwa wakiyashika, katika kipindi hicho, alikumbuka kila kitu.

    “Usiogope Erick. Nitakuwa nawe bega kwa bega” Bria alimwambia Erick alipomtembelea hotelini.

    “Utakuwa nami bega kwa bega? Kivipi?” Erick aliuliza.

    “Namini nitakwenda huko Iraq pamoja nawe. Kuna vitu vingi sana ningependa kujifunza kutoka kwako” Brian aimwambia.

    “Inamaanisha tutakwenda wote?”

    “Utanikuta huko, ila tutakuwa wote na kufanya kazi pamoja” Brian alimwambia Erick.

    Siku iliyofuata, safari ya kurudi Tanzania ikaanza. Kila mara alikuwa akiifikiria safari hiyo ya kuelekea nchini Iraq. Amani ikaonekana kutoweka moyoni mwake. Mwisho wa kila kitu ukaonekana kutimia.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Erick alifika nchini Tazania baada ya masaa thelathini na saba. Akaanza kuteremka ngazi pamoja na abiria wengine mpaka ndani ya jengo la uwanja ule. Baadhi ya wafanyakazi wenzake walikuwa wamekuja kumpokea wakiwa na mkewe.

    Uso wake haukuonekana kuwa na furaha, muda wote alikuwa akiifikiria safari ya kuelekea nchini Iraq, nchi ambayo aliiona kujaa damu. Akakumbatiana na mkewe, kwa mbali machozi yalikuwa yakianza kumlenga.

    “Usiogope mume wangu. Amini Mungu yuko pamoja nawe” Christina alimwambia Erck.

    “Naamini hilo”

    Erick alikaa nchini Tanzania kwa takribani wiki moja na ndipo safari yake ya kuelekea nchini Iraq ikaanza. Ndani ya ndege, Erick hakuonekana kuwa na furaha hata kidogo, kila wakati alikuwa na mawazo kupita kawaida.

    Hakujua kama angeweza kurudi salama nchini Tanzania, hakuamini kama angeweza kurudi na kumkuta mkewe akiwa amekwishajifungua. Alitamani kumuona mkewe kwa mara nyingine lakini uhakika wa kumuona tena haukuwa moyoni mwake.

    “Naomba unilinde Mungu, naomba unirudishe salama nyumbani. Naomba mkono wako unitangulie. Amin” Erick alijikuta akisali huku ndege ikianza kutua katika Uwanja wa Ndege wa Saddam uliokuwa katika jiji a Baghdad.

    Abiria wote waliokuwa ndani ya ndege wakaanza kuteremka, Erick akaanza kuyapitisha macho yake katika baadhi ya maghorofa yaliyokuwa yamejengwa katika jiji hilo ambalo alikuwa akilisikia tu katika vyombo mbalimbali vya habari, Baghdad.

    Majengo hayakuwa yakivutia sana kama yale ambayo aliyaona nchini Marekani, Uingereza, Uholanzi na nchi nyingine za Ulaya. Idadi kubwa ya watu ilikuwa ikionekana vizuri machoni mwake huku idadi hiyo wengi wao wakiwa wamevaa kanzu na vilemba vichwani.

    Erick akaanza kuelekea nje ya jengo la uwanja huo, kijana mmoja ambaye alishika bango lililoandikwa jina lake lilikuwa likionekana vizuri machoni mwake. Kwa hatua fupifupi zilizojaa haraka, Erick akaanza kumsogelea kijana yule ambaye akampeleka moja kwa moja mpaka katika teksi iliyokuwa nje.

    “Welcome to Baghdad City” Kijana yule ambaye alikuwa akindesha gari alimkaribisha kwa kutmia kingereza kilichojaa lafudhi ya kiarabu.

    “Thank you” Erick aliitikia huku macho yake yakiangalia nje.

    Gari lilikuwa likitembea kwa mwendo wa taratibu sana, idadi kubwa ya watu wengi ambao walikuwa wakiandamana mitaani huku wakiwa na mabango ndio ambao walisababisha foleni kubwa ya magari. Erick alibaki akiwaangalia waandamanaji wale pamoja na kuyasoma baadhi ya mabango ambayo yalikuwa yameandikwa kwa lugha ya Kingereza.

    Hadi kufikia hatua hiyo tayari Erick akaonekana kuanza kuogopa. Waandamanaji ambao walikuwa wameshika mabango ya kumkataa rais wa nchi hiyo bado walikuwa wakiendelea kuandamana huku mikononi wakiwa wameshika picha za rais huyo.

    Ingawa mabomu ya machozi yalikuwa yakipigwa lakini hakukuwa na mtu yeyote aliyeonekana kuogopa na kurudisha mguu wake nyuma, wote walikuwa wakisonga mbele kuwasogelea mapolisi ambao walionekana kuwa na hasira muda wote.

    Sala za Erick za kumuomba Mungu zikaanza tena. Alitamani waandamaji wale wasogee pembeni kwa ajili ya kulipisha gari lao lipite. Walichukua dakika kumi mpaka kuwapita waandamaji wale na baada ya kipindi kichache wakafika nje ya hoteli moja iliyoitwa Majifallus.

    “This is the hotel I was told to take you to (Hii ndiyo hoteli niliyoambiwa nikulete)” Kijana yule alimwambia Erck.

    Erick akaufungua mlango na kushuka garini na kisha kuanza kupiga hatua kuelekea ndani ya jengo la hoteli ile. Moja kwa moja akaanza kupiga hatua kuelekea sehemu ya mapokezi. Kila kitu alikikuta kikiwa kimewekwa tayari kwa ajili yake.

    “Thank you” Erick alimwabia dada wa pale mapokezi huku akiupokea ufunguo.

    Erick akaanza kupiga hatua kuzifuata ngazi za kuelekea katika ghorofa za juu. Wasiwasi bado ulikuwa ukiendelea kutawala moyoni mwa Erick, fujo ambazo alikuwa akizisoma katika magazeti hasa za maandamano tayari zilikuwa zimekwishaonekana.

    Huku Erick akiendelea kupandisha ngazi, akashtukia akishikwa bega kwa nyuma. Akageuka na macho yake kugongana na macho ya mtu ambaye wala hakuwa mgeni machoni mwake. Kwa haraka haraka akavuta kumbukumbu juu ya mtu yule kama alikwishawahi kumuona kabla.

    “Erick....” Mwanaume yule aliita.

    “Brian..”

    Wote, huku wakionekana kuwa na furaha wakaanza kuelekea katika ghorofa ya juu. Maswali mfululizo yalikuwa yakimjia Erick, hakuwa akifahamu sababu ambayo ilimleta Brian nchini Iraq, kila alipotaka kumuuliza, alisita kufanya hivyo.

    “Nilikuona tangu uwanja wa ndege, kila nilipojaribu kukuita, haukugeuka” Brian alimwambia Erick.

    “Ulijua kama nilikuwa naingia hapa leo hii?”

    “Ndio. Nilipewa taarifa na mkurugenzi wa CNN, Bwana Swan” Brian alijibu.

    “Umekuja kufanya nini huku?”

    “Kufanya kazi pamoja nawe. Natamani kujifunza mambo mengi kutoka kwako” Brian alijibu.

    “Na vipi kuhusu kazini kwako? Hauoni kama utatumia muda mrefu kuwa huku?”

    “Hilo si tatizo. Nimeomba ruhusa. Waliniruhusu kwa sababu tu nilikuwa nakuja kufanya kazi na mmoja wa waandishi aliyetumwa na shirika la CNN” Brian alijibu.

    Ukaribu wao ukaonekana kuanza kurudi kwa mara ya pili. Hakukuwa na mtu yeyote ambaye walikuwa wamemzoea nchini Iraq zaidi ya kuzoeana wenyewe kwa wenyewe. Ukaribu wao ukazidi kuongezeka kila siku, wakawa wakitoka pamoja na kwenda kufanya kazi pamoja mitaani, waliandika kila kitu ambacho walikiona kufaa kuandikwa katika vitabu vyao vidogo.

    “Nimefurahi kukutana nanyi. Mimi ni Mchungaji Joseph Terence wa kanisa la Salvation jijini New York. Huyu ni mke wangu, anaitwa Mary” Mwanaume mmoja alevalia suti alijitambulisha mbele yao.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Bwana Asifiwe” Mary alisalimia.

    “Amen” Wote wakajikuta wakiitikia.

    “Tumekuja hapa kwa kazi moja tu, tumekuja kufungua kanisa hapa Baghdad. Nafikiri kazi hii tutaifanya kesho pamoja na mke wangu” Mchungaji Joseph aliwaambia.

    ***

    Uongozi wa rais Yassin Idrisour ulikuwa ukiwakasirisha wananchi wote wa Iraq. Vita ambavyo vilikuwa vimetokea katika miaka kadhaa ya nyuma dhidi ya Wamarekani na Waingereza bado viliwaacha katika maumivu makali, maumivu ambayo hayakuwa na dalili yoyote ya kupona.

    Kila raia wa Iraq alikuwa akiwachukia Wamarekani na Waingereza kuliko mtu yeyote duniani, walitamani mataifa ya Marekani na Marekani yapotee ili nchi hizo zisiweze kuonekana katika uso wa dunia hii. Wanajeshi mbalimbali wa Kimarekani na Uingereza ambao walikuwa nchini Iraq kwa ajili ya kulinda amani walikuwa wakiuawa kila siku.

    Mauaji ya siri siri dhidi ya Wamarekani na Waingereza bado yalikuwa yakiendelea kila siku. Waandishi wa habari na watalii kutoka katika nchi hizo walikuwa wakikamatwa na kupotea katika mazingira ya kutatanisha. Hakukuwa na mtu yeyote ambaye alijua mahali ambako watu hao walipokuwa wakipelekwa, wapelelezi wa Kimarekani wa F.B.I na wale wa Uingereza walijitahidi kupeleleza lakini hawakuwa na jibu lolote katika upelelezi wao.

    Nchi ya Iraq ikaonekana kuwa chungu. Japokuwa mauaji yalikuwa yakishamiri nchini Iraq lakini Wamarekani na Waingereza hawakukoma kabisa kuingia ndani ya nchi hiyo iliyoonekana kujaa damu.

    Rais Yassin alionekana kuwa kama kibaraka wa nchi hizo, kila siku alikuwa akiwatetea. Alipokuwa akiongea na vyombo mbalimbali vya habari nchini Iraq, alizidi kuutetea uwepo wa Wamarekani nchi humo, uwepo ambao aliutetea kwamba ulikuwa ni wa kuhakikisha amani nchini humo.

    Kila siku Wananchi wa Iraq walikuwa wakiandamana kutaka rais huyo atoke madarakani, hawakumtaka rais ambaye alionekana kuwa karibu na Wamarekani ambao walikuwa wamewapa vidonda visivyokuwa na uhakika wa kupona mioyoni mwao.

    Waliwapoteza ndugu, jamaa na marafiki zao wa karibu katika vita ambavyo vilikuwa vya kumtafuta gaidi ambaye alikuwa ameitikisa dunia katika kipindi hicho, Allabdullah Massoud. Uwepo wa Mmarekani ukaonekana kuwa ghadhabu katika maisha ya kila mwananchi wa Kimarekani.

    Ingawa Wamarekani wakishirikiana na Waingereza walijitahidi kuijenga nchi hiyo lakini hakukuwa na mtu yeyote ambaye alionekana kuwa na upendo na Wamarekani hao. Chuki dhidi ya Wamarekani ilikuwa ikiongezeka kila siku, mtoto alipokuwa akikua, alijikuta akiwachukia Wamarekani pasipo sababu yoyote ile.

    Watu walipigwa na mabomu ya machozi mitaani huku wengine wakipigwa na risasi za moto lakini hakukuwa na mtu yeyote ambaye alionekana kupiga hatua kurudi nyuma katika maandamano ambayo walikuwa wakiyafanya kila siku.

    Walionekana kuwa radhi kupoteza maisha yao katika maandamano hayo lakini ili mradi Wamarekani hao waondoke nchini humo. Mabango yaliyokuwa yakimtaka rais wa nchi hiyo atoke madarakani bado yalikuwa yakionekana katika kila makundi ya maandamano nchini Iraq.

    “Ni lazima tuwaue Wamarekani wote waliokuwa wamepanga katika hoteli nchini hapa” Baadhi ya Waarabu ambao mara kwa mara walikuwa wakionekana kuwachukia Wamarekani walisema.

    Msako wa Wamarekani ukaanza kufanyika kimyakimya. Hawakutaka taarifa hizi zijulikane na mtu yeyote ambaye alikuwa nje ya kundi hilo lililopewa kazi ya kuwamaliza Wamarekani. Wamarekani ambao walikuwa katika hoteli katika miji mingine walitekwa.

    Kazi ya kuwateka Wamarekani waliokuwa wakiishi katika hoteli zilizokuwa ndani ya jiji la Baghdad ikaanza mara moja. Waarabu wakaanza kuingia katika kila hoteli na kuanza kuwatafuta Wamarekani. Wamarekani wengi walikamatwa na kupelekwa sehemu isiyojulikana.

    Kila kitu ambacho kilikuwa kikiendelea nchini Iraq kilifanyika kimyakimya. Hakukuwa na mtu yeyote ambaye alifahamu juu ya kile ambacho kilikuwa kinaendelea mahali hapo. Kila siku Wamarekani walikuwa wakitekwa na kupelekwa katika sehemu zisizojlikana kabisa.

    “Hoteli zote tumemaliza mkuu. Tumewapata Wamarekani mia nane” Bhazir alimwambia kiongozi wao, Ashraf

    “Mmekwenda katika kila hoteli?” Ashraf aliuliza.

    “Ndio Mkuu”

    “Na hapa Baghdad, mmemaliza hoteli zote?”

    Bhazir hakutoa jibu lolote lile, alikaa kimya kwa muda huku akionekana kufikiria kitu. Baada ya sekunde kadhaa, akauinua uso wake na kumwangalia kiongozi wake.

    “Kuna hoteli moja hatukuingia” Bhazir alijibu.

    “Hoteli gani?”

    “Majifallus Hotel”

    “Kwa nini?”

    “Kuna ulinzi mkubwa mkuu”

    “Hata kama kuna ulinzi, hakikisheni mnakwenda na kuwateka Wamarekani wote. Kama mkiona mnashindwa, tumieni bunduki” Kiongozi yule alisema.

    Kwa haraka sana pasipo hata kupoteza muda wowote ule, Bhazir akatoka ndani ya chumba kile na moja kwa moja kuanza kupiga hatua kuelekea nje. Akawachukua vijana kumi waliokuwa na bunduki 

0 comments:

Post a Comment

Blog