Search This Blog

Sunday 22 May 2022

BORN TO DIE - 2

 







    Simulizi : Born To Die

    Sehemu Ya Pili (2)

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kwa nini umesema hivyo Vanee.” Peter aliuliza tena na kumfanya Vanessa atabasamu kwa lile tabasamu lake hafifu.

    “Yaani umeongea kama baba anavyopenda kuniambia. Na hilo jina unavyolifupisha ni kama baba vile. Yaani wakati unaongea nikahisi kama nipo nyumbani na baba.” Vanessa aliongea huku akizidi kuchanua tabasamu na kumfanya Peter naye afate tabasamu hilo kwa kulijibu.

    “Tunachojaribu mimi na baba yako ni kukushauri na si kukulaghai. Achana na kisasi na anza maisha yako bila moyo wenye nyongo iliyotumbuka.” Peter alizidi kushauri.

    “Basi nimekusikia baba, haha haa.” Vanessa alimjibu Peter na kucheka cheko ambayo ilijaza ahueni katika kichwa cha Peter Madira.

    “Ha ha haaa, eti baba. Haya bwana. Ehee, embu nimalizie hadithi ya mama yako basi. Maana ni kama naangalia filamu ya kusisimua sana.” Peter alitoa ombi ambalo Vanessa hakuwa na kipingamizi kwa kulitimiza huku akiweka utani mwingi kabla hajatimiza.



    “Na wewe nawe, wajidai unapenda story. Si umtafute Frank Masai akupe simulizi ya kukutoa machozi ya My Rose au Duka La Roho.” Alitania Vanessa huku akikaa sawa kwa ajili ya kuendeleza simulizi ile.

    “Ha ha haaa, kumbe na wewe unamkubali yule jamaa eeh. Ni kichwa.” Peter alitoa sifa zake kwa mwandishi nguli wa riwaya, Bwana Frank Masai.

    “Yule tena. Mi sijawahi kumuona kama anakosea.” Vanessa naye aliongeza ndimu kwenye kachumbari na kuifanya mboga ile waliyokuwa wanaichanganya ipendeze kwa upande wa ladha.

    Furaha na utani vikaendelea lakini mwisho wake ulikuwa ni Vanessa kumalizia simulizi ya jinsi mama yake alivyouawa kikatili na mtu aliyemuita rafiki kipenzi.



    “Yule rafiki mnafki wa mama akashuka toka garini na kwenda mbele ya mama na kisha akaanza kuongea maneno yaliyomkaghadhabisha mama. Maneno hayo yalimfanya mama amtemee mate usoni yule mwanaharamu. Na hapo ndipo nilishuhudia jambo la ajabu katika maisha yangu, jambo ambalo hadi leo picha yake ipo kichwani.

    Nakwambia ukweli Pity, sikuweza kufanya chochote kwa mwezi mmoja na nusu baada ya kushuhudia tukio lile. Nilikuwa kama nimepararaizi mwili mzima, hadi kope. Sikuweza kufumba macho wala kuyachezesha. Hiyo yote ni sababu ya lile tukio.

    Ni tukio la ajabu sana kuliangalia hasa kwa umri niliokuwanao, lakini nashukuru lile tukio ndio limenipa ujasiri leo hii nasimulia bila kutoa machozi wala kuweweseka. Ipo siku yule mama atalipa tu!” Vanessa aliongea kwa uchungu huku macho yakianza kubadilika na kuwa mekundu.



    “Baada ya kutemewa mate na mama, yule mwanamke alifanya ishara ya kumuita mtu toka kwenye ile gari. Hapo akatoka mwanaume mmoja aliyejazia mwili wake, kiunoni kaweka jambia moja refu sana.

    Hakika yule mtu alitisha kwa kumuangalia tu! Achana na matendo anayoyafanya.

    Yule rafiki mnafki, akamnong’oneza kitu jitu lile la miraba minne. Jitu lililokuwa limevalia sare za jeshi ya nchi kavu.

    Baada ya kumaliza kumnong’oneza, yule mama alisogea pembeni kama anakuja upande tuliojificha sisi. Akaangaza macho yake pande zote, kisha akapaza sauti yake.

    “Najua mnaona yote yanayoendelea. Mimi sina haja na nyie, nia yangu ni huyu hapa na nimempata. Kwa usalama wenu, badala ya kufikiria maisha ya huyu mshenzi wenu, ni bora mfikirie maisha yenu ya baadaye.



    Nawapeni nafasi ya kupotea kabisa katika nchi hii. Kaanzisheni maisha katika nchi nyingine, mkionekana katika nchi hii, mtakuwa kiteweo cha cha mbwa kama huyu mwanamke mbele yenu.”

    “Yule mama aliongea hayo kisha akampa ruhusa yule baba sura mbaya.” Vanessa alizidi kusimulia mkasa uliowakuta na safari hii Peter alishuhudia chozi likimtoka mwanadada yule jasiri.

    Peter akachukua nafasi hiyo kumfariji kwa kumlaza katika mapaja yake na kuanza kuchezea nywele zake.

    “Yule baba akachomoa jambia lake, kisha akaenda nyuma ya mama na kuzivuta kwa nguvu kwenda nyuma nywele za mama. Mama akawa kama ameangalia juu. Hapo alikuwa kampa nafasi ya kukata shingo yule baba.



    Mama akachinjwa kama ng’ombe. Alichinjwa kama kuku mama yangu, Pity. Mama alichinjwa bila sababu yoyote.

    Kisha yule baba alinyoosha mkono juu huku kakamata kichwa cha mama. Alipoushusha mkono, alitupa kile kichwa kwenye lile kundi la mbwa. Mbwa wakala kichwa cha mama, wakajilamba kwa utamu wa damu ya mama yangu.” Vanessa aliongea kwa majonzi huku machozi yakizidi kuchukua nafasi katika macho yake.

    “Pity. Nilishindwa kupiga hata kelele. Nilibaki nimesimama wima nisijue nataka kufanya nini. Baba naye alikuwa vivyo hivyo.



    Alikuwa kaganda akishindwa kuamini kile alichokuwa anakiona.

    Hadi anarudiwa na fahamu, mimi nilishakuwa kama mnala wa barafu. Siwezi kufanya chochote.Ikabidi aninyanyue kimyakimya na kutoka kwenye kichaka kile. Tulipoelekea sikupajua tena. Lakini mama yangu alikufa hivyo Pity. Mama alichinjwa na rafiki yake kipenzi.” Vanessa alimaliza kumuhadithia Peter na kisha akafuta machozi yaliyokuwa yanatoka katika macho yake.





    Lakini mama yangu alikufa hivyo Pity. Mama alichinjwa na rafiki yake kipenzi.” Vanessa alimaliza kumuhadithia Peter na kisha akafuta machozi yaliyokuwa yanatoka katika macho yake.

    “Pole sana Vanee. Hayo ni mapito tu. Ipo siku MUNGU atakulipa kwa ubaya uliofanyiwa. Cha msingi muombe sana yeye.” Peter alishauri na kumfanya Vanessa ashushe pumzi ndefu kama mwanariadha aliyetoka kukimbia mbio za ndefu.

    “Pity, maisha ni njia tu. Hata kama hutaki kuiona, utaipita. Naamini ipo siku kuna mtu atakuja kumaliza kile nilichokianza katika moyo wangu.” Vanessa aliongea na kumfanya Peter akae kimya akitafakari juu ya maneno yake.

    “Sitakufa bila kumuona yule mama akitekea.” Vanessa akamalizia kauli yake na kunyanyuka pale alipokuwa amejilaza, na kisha alitoka nje na kilichosikika baada ya kutoka nje, ni mlio wa gari lake ikiashiria anaondoka tena bila kumuaga mwenyeji wake.



    Baada ya Vanessa kuondoka nyumbani kwa Peter bila kuaga, Peter akaamua kujilaza chali kitandani kwake huku akiwa hana hata muda wa kutoka nje na kuangalia yule mwanadada kaenda wapi. Hakuwa na haja ya kufahamu hilo kwa kuwa alijua Vanessa anahasira kwa wakati ule. Hasira hizo zilimpelekea kuchukua maamuzi magumu ya kuondoka bila hata kuaga.

    Wakati amelala pale kitandani huku anaangalia paa la nyumba ile aliyopangisha, alijikuta akitabasamu peke yake na kutikisa kichwa huku akitoa mlio fulani kwenye mdomo wake kama wa kusikitika.

    “Ama kweli duniani kila mtu anahistoria yake. Baba hakukosea haya maneno.” Alijisemea Peter baada ya kutuliza akili yake.

    Kauli hiyo aliwahi kuambiwa na baba yake wakati yupo hai. Na Peter siku zote alipenda kuweka maneno ya mzee wake hai. Peter aliishi kwa maneno ya baba yake.



    “Kila binadamu anahistoria yake katika dunia hii. Yupo mwenye historia ya kuhuzunisha, mwingine ya kuchekesha na mwigine ya furaha. Lakini zote hizo ni historia za maisha yao.

    Kamwe usijione mwenye historia mbaya hadi ukafikia hatua ya kumkufuru MUNGU au kumuuliza kwa nini wewe huku ukigonga kifua chako kwa ngumi kana kwamba MUNGU kakuacha. Kamwe usifike huko.

    Wapo wenye historia ambayo ukiisikiliza mara moja pekee, hutotaka kuisikiliza tena kwa jinsi ilivyojaa visa na mikasa, machozi na maumivu, tabu na masumbuko, shida na mahangaiko ya kumfanya mtu huyo asifanye chochote. Lakini bado anaamini kuwa MUNGU yu upande wake, anaamini kuwa MUNGU anamuona na ipo siku atampa anachokililia na kukiomba.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Iache historia yako iwe yako. Ya mwingine iwe fundisho kwako, iwe sehemu ya kujifunza cha kufanya na si kukaa na kujiona kuwa wewe ndiye mwenye historia kali kuliko wenzako. Wapo walionazo kali zaidi yako, lakini nao pia wanawatu ambao wakiwasimulia historia zao, wanajiona cha mtoto.” Ni maneno ya Hayati Mzee Madira, Baba mzazi wa Peter.

    Peter aliyakumbuka maneno hayo wakati kalala kitandani kwake na wakati yanaendelea kutiririka katika ubongo wake, alijikuta akibebwa na usingizi ambao ulikatika baada ya saa moja.

    Akatoka na kuangalia mazingira ya nje na wakati huohuo, akachukua jukumu la kujipatia chakula cha jioni, na kisha alikaa mahala kwa ajili ya kuisubiri usiku.



    ******



    Kesho yake ilikuwa siku nyingine ambayo kwa Peter iliendelea kuwa tofauti. Kiasi cha fedha alichopatiwa na Vanessa, kiliweza kumsukuma kimaisha kiasi fulani na kuanza kusahau maisha ya kutembea mwendo mrefu kwa kutumia viungo vyake vya mwili.

    Kama kawaida, baada ya kufika katika chuo/shule anayosoma, pale nje alikutana na sura ya mrembo aliyebadili mwelekeo wa maisha yake kwa siku kadhaa. Yaani ndani ya siku zile alizokutana na Vanessa, hata milo ilienda vizuri.

    “Hey Pity. Mambo.” Vanessa alimsalimia Peter huku akimfuata kule alipokuwa anatokea.

    “Poa. Mzima wewe.” Peter alijibu salamu ya kimwana yule huku akichanua tabasamu la kitanashati kwa mrembo.

    “Poa tu. Ila samahani kwa yal .........” Vanessa hakumaliza kauli yake, Peter alikuwa ameweka mkono wake mdomoni kwa mrembo kama kumkataza asifanye alichokusudia.



    “Nafahamu Vanee. Naelewa sababu ya wewe kufanya vile. Hata ningekuwa mimi, ningefanya vile. Hasira na dukuduku ulilonalo, unahaki hata ya kujikata kiungo cha mwili wako. Lakini kitendo cha kuondoka bila kuaga, kilikuwa ni kitendo cha afadhali kuliko ungejikata kiungo chako.” Peter aliongea na kumfanya Vanessa atabasamu.

    “Nashindwa cha kusema,” Vanessa aliishia kusema hayo baada ya tabasamu lake.

    “Usijali Vanee. Twende darasani sasa.” Peter alikata shauri na kuelekea darasani.

    Walipoingia kila mmoja akachukua nafasi ambayo kila siku huitumia. Na hapo masomo ya siku nzima yakaendelea.



    *****



    Urafiki kati ya Vanessa na Peter uliendelea kutanuka kila kukicha. Nyuso zao zilitaliwa na furaha kila mara pale walipokuwa pamoja. Hakuna ambaye hakukaukwa na tabasamu pale walipokuwa pamoja.

    Licha ya hayo yote kuendelea kutokea, hakuna hata mmoja aliyewahi kumtamkia mwenzake kuwa anamuhitaji, yaani anataka wawe wapenzi.



    Moyo wa Vanessa ulishampenda kitambo sana Peter. Lakini tatizo lilikuja pale alipotaka kuzipeleka hisia zake. Kila alipotaka kumwambia kuwa anampenda Peter, alijiona kama mwenye makosa. Alihisi Peter atamuhisi vibaya, hasa ukizingatia tamaduni za Kiafrika, wewe mwanamke huwezi kumtongoza mwanaume. Hilo likamtesa Vanessa, kila alipotaka kusema kinachomsibu, kikwazo cha atanifikiriaje, kinachukua nafasi kichwani kwake.

    Kwa upande wa Peter, moyo wake pia ulikuwa umezama ndani ya penzi zito kwa yule kimwana. Kila kukicha pendo hilo ndani ya moyo wake lilikuwa linakamata nafasi kubwa kuliko hata maisha yake ya kawaida.

    Lakini naye alikuwa anatatizo lake binafsi. Hakutaka kumwamini Vanessa kirahisi hivyo, hakutaka kuamini kuwa Vanessa ni mtu mwema. Moyo wake ulihisi Vanessa yupo pale kama mpelelezi tu, muda wowote anaweza kumgeuka au kumfanya chochote. Uhaba huo wa fikra, ukatafuna nafsi ya Peter. Kupenda, anapenda, lakini anayempenda anamuogopa. Ataishi vipi? Ikabaki kuangaliana pekee pale walipokutana.



    *****



    Miezi ikaenda na kupotea na hatimaye ule mwezi wa kumaliza masomo waliyoyachukua, ukawadia.

    Siku hiyo hawa marafiki wanaopendana walikuwa katika hali inayofanana. Wote mioyo yao ilikuwa inawauma sana kuachana, wote walitaka wawe pamoja katika maisha yao ya kila siku. Lakini ni vipi watakuwa pamoja kama mawazo yao yanaingilia hisia zao? Watakuwa pamoja kivipi kama fikra zao zinafunga pingu mioyo yao iliyopendana? Suala hilo ndilo lililokuwepo kwa wakati huo.

    “Pity, leo ndio mwisho wa masomo yetu. Kwa hiyo sikuoni tena?” Vanessa alimuuliza Peter kabla hawajaingia kwenye chumba cha kufanyia mtihani wao ambao ulikuwa unahusu zaidi mambo ya kompyuta.



    Ni swali kama la kitoto ukikaa ukilifikiria, lakini utoto huo ndio unaomuumiza binti mrembo, binti mwenye kila sifa ya kuitwa anavutia kitabia na sura.

    Peter alitabasamu, tabasamu lake la kitanashati kisha akamjibu kifupi tu.

    “Usijali Vanee. Ngoja tutoke.” Hicho ndicho alichojibu Peter.

    Wakaingia darasani na kilichofuata hapo ni kumsubiri msimamizi aingie ili waanze kufanya mtihani unaowakabiri.

    Wakati wanaendelea kusubiri, ndipo Peter aliamua kugeuka nyuma mara moja na kumuangalia Vanessa. Hapo macho yao yalikutana na kwa wale wakongwe wa mapenzi wangewaona, wangekwishasema mioyo yao imeongea jambo tamu la mapenzi baada ya macho kukutana.



    Matabasamu yaliyochanuka midomoni mwao, hakika yalisema kila kitu.

    Peter akageuza shingo na kuilekeza kule ilipokuwa mwanzo. Hapo akaanza kukumbuka maneno ya baba yake kipenzi, Mzee Madira.

    “Maisha ni matamu sana pale unapopata mpenzi anayekupenda nawe ukampenda. Ila huwa machungu sana kama yule uliyempenda akawa hakupendi, yaani hayupo kichwani kwako kabisa. Hiyo huwa inauma sana tena sana.

    Hakuna afahamuye moyo wa mwenzake kwa kumuangalia usoni. Yawapasa mtambue hilo wanangu.” Maneno hayo aliyatoa Mzee Madira wakati yupo na watoto wake wote wa kiume. Bado yaliendelea kukaa kichwani mwa Peter.



    “Ni vipi utamtambua akupendaye? Hilo ni swali ambalo wengi wanajiuliza. Lakini jibu lake ni dogo sana, mpe nafasi katika maisha yako. Muache aingie katika maisha yako, hapo ndipo utajua kama unapendwa au kaja kucheza na hisia zako.

    Kama kaja kwa ajili ya kucheza na hisia zako, muache haraka kabla mambo hayajawa mabaya zaidi. Kamwe usithubutu kumng’ang’ania mtu asiyesahihi katika maisha yako. Na njia ya kumpata aliyesahihi, ni wewe kuachana na yule asiyesahihi. Hata kama umempenda kiasi gani, achana naye kama si sahihi.

    Kama waona ndiye sahihi, mpe nafasi hiyo. Moyo ndio kila kitu katika mahusiano. Kama moyo utasema hapana, basi mwili nao utakataa.



    Mpende yule anayekujali na kukupenda. Na usiogope kupenda kwa kuhofia maumivu ya kuachwa au chochote kile. Penda kadiri ya uwezavyo, ukiachwa si tatizo. Rekebisha sababu za kuachwa kisha ingia penzini tena. Endelea kupenda zaidi na zaidi, usikate tamaa.” Baada ya maneno hayo kupita kichwani mwa Peter, alitabasamu kama kawaida yake na kisha akageuka nyuma tena na kumuangalia Vanessa.

    Macho yao yakakutana tena, hapo Peter alichukua nafasi hiyo adimu kwa kupepesa midomo yake. Ni kama alikuwa ananong’oneza lakini midomo yake ulipaswa uisome ili ufahamu alichozungumza.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “I Love You.” Ndicho kitu kilichopepeswa katika midomo ya Peter.

    Vanessa aligeuka nyuma na pembeni ili kuangalia kama kuna mtu aliyeona kilichotokea. Kwa bahati mbaya kuna mmoja aliona, na huyo naye ni kama alichochea tu.

    “Mjibu sasa mwenzako.” Jamaa huyo aliongea kwa sauti ambayo ni Vanessa ndiye aliyeweza kuisikia na kuelewa alichomaanisha.

    Vanessa akageuka mbele lakini alikuta Peter kishageukia kompyuta yake na hakugeuka tena hadi pale msimamizi alipokuja na kutoa mtihani husika.

    Mtihani ukafanyika na kumalizika na hatimaye wakatoka nje.

    “Pale uliniambiaje?” Vanessa alimuuliza Peter baada ya kutoka nje na kumvutia mahala penye mkusanyiko mdogo wa watu.

    “Nakupenda. Vipi, hutaki kupendwa na mimi?” Peter alijibu na kukandamiza swali.



    Vanessa akakumbwa na haya kiasi fulani. Akashindwa ajibu nini na afanye nini baada ya maneno yale kadhaa toka kwa Peter.

    “Mapenzi ni njia moja ya kuipitia katika maisha ya kila mwanadamu. Unaambiwa katika kundi la watu kumi hapa duniani, watu wasiopungua nane, ni lazima waje kupenda. Moyo wangu unasema ni wewe ndiye nikuhitajiye kwa sasa. Wewe ndiye uwezaye kuusulubu moyo wangu kwa pendo lililopandikizwa ndani yake. Kama ukinipa nafasi ya kuwa na wewe, hakika moyo wako hautakuwa umefanya kosa.” Peter alitema cheche ambazo zilivamia vizuri na kukita ubongoni mwa Vanessa aliyekuwa anaangalia pembeni kwa aibu wakati maneno hayo yanatokwa mdomoni mwa Peter.



    “Vanee,” Peter alimuita Vanessa baada ya kuona kimya kimetanda.

    “Pity. Ni kama ndoto. Ni kama ndoto niliyokuwa naiota wakati nimelala halafu nikaamka na kukuta ni kweli imetokea. Nimesubiri kwa muda mrefu muda kama huu ili yatimie, na kweli yametimia. Moyo wangu ulipokuwa unahitaji kufika, leo umefika.

    Pity, u ndoto yangu. U ndoto iliyokuwa inautesa mtima wangu. Nashukuru umekuja kuuponya. Nakupenda sana Pity.”Vanessa alimaliza maneno yake na kwenda kumkumbatia Peter kwa nguvu huku Peter naye akijibu mapigo kwa kukubali kumbate lile kwa hali mali.



    Ukurasa wa mapenzi kwa vijana wale ukawa umefunguliwa rasmi. Hakuna aliyependa kumuacha mwenzake aende mbali, na hakuna ambaye alijisikia vizuri mwenzake kuwa mbali na upeo wa macho yake.

    Kwa hali hiyo, Vanessa aliamua kumpa taarifa baba yake juu ya Peter. Na bila kuchelewa, Baba wa Vanessa, alituma makachero wake kwa ajili ya kufuatilia nyenendo za Peter. Naye hakukaa nyuma, akaingia mtandaoni kuhakikisha taarifa alizopewa na mwanaye kuhusu Peter Madira.



    Aliporidhika na taarifa alizokuwa anazitafutafuta, alimuita mwanaye mpendwa na kumtaka amlete Peter nyumbani kwake ili wakutane na waongee mawili matatu.

    Binti kwa furaha, alienda kwa Peter na kumpa ujumbe huo. Peter naye hakuwa na ubishi kwa kuwa alishapewa taarifa hizo na Vanessa toka kitambo. Akafanya kama alichokusudia kufanya, huku penzi zito alilokuwa nalo kwa Vanessa, likimsukuma kufanya hivyo.



    Ikafika siku ambayo Peter alipaswa kwenda kumuona Mzee Gomez, Baba mzazi wa Vanessa. Siku hiyo ilikuwa ni tabasamu pekee ndilo limetawala katika nyuso za hawa waliopendana (Vanessa na Peter). Pale Peter alipokaribishwa ndani ya jumba kubwa, jumba lililojengwa kwa ramani za Wareno na Wahispani, Peter alishindwa cha kusema juu ya jengo hilo. Alibaki akipepesa macho huku na huko kama anayetafuta mjusi anayekoroma usiku.





    “Nadhani wewe ndiye Peter Madira.” Sauti nzito ilikoroma kwa kumuuliza Peter ambaye akili yake yote ilihamia kwenye kutafakari lile jengo kubwa kama Kasri ya Jeshi. Hata pale Mzee Gomez alipotoka chumbani kwake na kuja kuonana naye, yeye Peter hakusikia chochote.

    “Ndio mimi mzee, shikamoo,” Peter ni kama aliyegutuka toka usingizini. Akasimama na kumsalimia Mzee Gomez.

    “Marahaba kijana. Upo penzini na mwanangu, nakosea?” Mzee Gomez hakutaka kuchewelesha alichokusudia kukiongea, moja kwa moja akaingia kwenye maongezi.

    “Ndiyo Mzee.” Peter akajibu kwa heshima huku bado kasimama mbele ya kochi alilokuwa kakaa mwanzo.



    “Have a sit (Chukua nafasi/ Kaa).” Mzee Gomez alitoa ruhusa ya Peter kukaa huku akimuonesha kwa mkono sehemu husika.

    “Sitaki sana kujua ni nini kilichosababisha wewe kuwa na mahusiano na mwanangu, ila nachotaka kukwambia uwe makini sana na maisha haya. Kaniambia kila kitu kilichokusibu, na mimi mwenyewe nimefatilia na kugundua kuwa ni kweli. Tafadhali, huyo ni mwanangu, sitaki kumuumiza na ndio maana nimemsikiliza ombi lake.” Mzee Gomez aliendelea kutoa rai, huku Peter akiwa kichwa chini kuonesha heshima na maneno yale yanamuingia vizuri.

    “Nachotaka kujua ni malengo yako kwa mwanangu. Umepanga nini katika mahusiano yenu na mwanangu.” Swali likatua kwa Peter.

    “Nachojua nampenda sana Vanessa, nampenda sana mwanao. Kila lengo jema kwa mwanao, mimi ninalo. Sitasita kufa ili kumuokoa, na sitamwacha popote pale ambapo atakuwa amegota. Nitamkumbatia katika shida, nitambusu kumpa faraja pale aumwapo, na nitahakikisha furaha yake haikauki pale awapo na mimi. Ni yeye pekee aliyeirudisha furaha yangu iliyopotea kwa muda mrefu, nailipa kwa wema, na kamwe sitafanya kinyume na matarajio yetu.” Peter aliongea kwa makini huku akimtazama mzee yule mzungu ambaye alikuwa kagotesha macho yake katika paji la uso la Peter.



    “Maneno mazuri na ya kumfariji yeyote ambaye hajui maisha ya sasa hivi. Maisha yaliyojaa uhuni na ujinga uliotukuka. Sitaki sana kuyafatilia maneno yako, ila naomba uyatimize hayo uliyoyatamka. Nitakuwa nawe bega kwa bega kwa hayo uliyokusudia.” Mzee Gomez alimaliza kuongea na kisha bila kumpa nafasi Peter, alinyanyuka na kuelekea kilipochumba chake. Lakini kabla hajatoka pale sebuleni, aligeuka nyuma haraka kama aliyesahau kitu.

    “Pia nimeonelea uje ukae hapa nyumbani ili tuweze kusaidiana zaidi. Kule unapokaa ni mbali sana. Sipendi mwanangu awe wa kufunga safari kila kukicha kuja kwako. Nakuomba uje ukae hapa. Pia ukiwa hapa, utakuwa na fursa ya kufanya mambo yako na kuna kazi ambayo nadhani itakufaa sana.” Mzee Gomez aliongea huku akimwangalia Peter.

    Peter hakuwa na jinsi kwani alichokisema mzee yule kilikuwa na maana sana katika usalama wake yeye Peter na usalama wa Vanessa. Hivyo bila kusita alikubaliana na Mzee Gomez na tendo hilo likatekelezwa haraka iwezekanavyo.

    Ndani ya siku tatu, tayari Peter alikuwa kahamia kwa Mzee Gomez na kama furaha ya mtu huletwa na mtu mwingine, hakika kwa Vanessa neno hilo lilitimia. Akawa hatoki nje wala kwenda mahala, uwepo wa Peter ulisababisha hayo yote.



    Mzee Gomez alishukuru sana kwa hilo, kwani sasa kazi zake alizifanya kwa uhuru sana. Mtoto wake alikuwa hatoki hovyo nje, hivyo ingekuwa vigumu sana kwa Vanessa kutekwa. Nyumba waliyokuwa wanaishi, ilikuwa na ulinzi wa kutosha, hivyo Mzee Gomez hakuwa na wasiwasi katika kuvamiwa kwa familia yake.

    Kuna baadhi ya watu ambao walikuwa wanakuja pale nyumbani kwa akina Vanessa. Wao walijitambulisha kama walimu waliotumwa na Mzee Gomez. Hao kazi yao ilikuwa ni kumfundisha Peter mambo ya Jiografia. Peter alijifunza kusoma rada pamoja na ramani na pia kutumia dira na mambo mengi mengine yahusuyo Jiografia.



    *****

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mwaka ukakatika bila kashikashi yoyote. Licha ya Peter kuwa pale nyumbani kwa mwaka mzima, hakuwa akijua kazi halisi ya Mzee Gomez. Aliopomuuliza Vanessa kazi ya baba yake, Vanessa alimjibu kuwa anachukua malighafi za nchi ile ya Senegal na Afrika kwa ujumla kisha anaenda kuziuza nchi za Ulaya na Amerika.

    Mali kama meno ya tembo, ngozi za wanyama mbalimbali na madini, ndivyo Vanessa alivyomwambia Peter kuwa baba yake anaviuza.

    Kwa upande wa nchi ile ya Senegal, hali ilikuwa tete kila kukicha. Mapigano kati ya Serikali na Waasi yalikuwa yanakuwa kwa kasi kila siku. Kile chama ambacho walikuwamo Mama Madira na mwanaye wa kwanza, ndicho kilikuwa kimekamata madaraka sasa.

    Kikawa kimeshikilia mpini huku wale viongozi wa zamani wakiwa wamekamata makali. Mpini ukivutwa kwa nguvu, basi yale makali huwakata vidole au mkono kabisa.

    Chama kile kikawa kinawaaua kinyama wale viongozi wa zamani ambao walikuwa madarakani. Kila kukicha hali ilikuwa ngumu kwa viongozi waliopita pamoja na familia zao. Hata wale wananchi waliokuwa wanakishabikia chama tawala cha zamani, nao wakawa wanakumbana na maswahibu ya kuuawa au kufirisiwa. Kwa kifupi nchi ilichafuka sana.



    Kuchafuka huko, ndiko kulikoanzisha mapigano ya wenyewe kwa wenyewe. Mapigano baina ya Serikali na Waasi wa nchi hiyo. Waasi waliokuwa hawataki kuona uonevu ukiendelea nchini kwao.

    Haileweki ni nini chanzo cha Waasi wale kuibuka, lakini ukweli ni kwamba kila kitu kilishapangwa kutokea.

    Mataifa makubwa duniani yalikuwa mstari wa mbele kuchochea vurugu na vita nchini Senegal. Na wao ndio waliochukua jukumu la kuendeleza kile kikundi cha Waasi.

    Wakawa wanawapa silaha za maangamizi kila wakipata fursa hiyo. Silaha nyingine hazikuwahi kuonekana katika upeo wa macho ya watu, lakini nchini Senegal, zilionekana. Silaha hizo zikawa kama za majaribio kwa Waafrika wasio na hatia. Mauaji yasiyo na idadi kila siku, ikawa ndio furaha kubwa kwa mataifa yale. Waliona silaha zao zinafanya kazi ipasavyo.



    Mzee Gomez licha ya kuwa anauza malighafi za Afrika, lakini pia alikuwa anajihusisha katika usambazaji wa silaha hizo kwa Waasi wa barani Afrika. Hata kifo cha mkewe, kilitokana na kazi hiyo. Ilikuwa ni kama onyo baada ya kushtukiwa kuwa anasambaza silaha za maangamizi katika nchi ya Kongo.

    Vanessa alijua kazi ya baba yake, lakini hakutaka kuwa wazi kwa Peter. Mzee Gomez akazidi kupeleka malighafi nje ya Afrika, na kisha aliingiza silaha pamoja na kiasi kikubwa cha fedha. Silaha hizo ndizo alizozipeleka kwa Waasi wa Senegal na kuvifanya vita nchini humo kuzidi kupamba moto.



    ****



    Peter na Vanessa, mapenzi yao yalizidi kutanuka kila kukicha. Furaha kubwa ilikuwa inaendelea kukua mioyoni mwao. Hakuna aliyetaka kukatishwa furaha hiyo, na siku zote waliamini hakuna atakayeikatisha zaidi ya MUNGU.

    Lakini maisha yamegubikwa na pande nyingi sana katika dunia hii ya sasa. Unaweza kuishi kwa furaha sana siku zote za maisha yako, lakini kuna wakati ni lazima upite katika huzuni japo kidogo ndipo ukamilishe furaha hiyo.

    Wakati wapenzi hawa wapo katika jumba la Mzee Gomez ambaye alikuwa katoka usiku huo, mara simu ya Vanessa iliita na alipoangalia, alikuwa ni baba yake.

    “Haloo Baba,” Vanessa alipokea kwa furaha simu ya baba yake.



    “Tokeni haraka hapo nyumbani. Ingia chumbani kwangu, fungua kabati na toa ‘Briefcase’ kisha tokeni humo ndani kwa kupitia kule ‘stoo’.” Sauti ya Mzee Gomez ilimwambia Vanessa huku ikionesha wazi ilikuwa katika wakati usio na masikhara.

    “Baba kuna nini?” Vanessa aliuliza.

    “Si muda wa maswali. Fanya nilichokwambia. Mpe simu Peter.” Mzee Gomez aliongea na haraka Vanessa alimpa simu Peter na yeye kwenda kuchukua alichoambiwa.

    “Peter. Mwanangu sasa nakukabidhi wewe. Wewe ndiye mtoto wa kiume. Nipo katika wakati mgumu huku nilipo, sidhani kama nitatoka salama. Kuwa baba wa mwanangu kwa sasa, nakupa majukumu hayo.Kwenye hiyo ‘Briefcase’ kuna maelezo ya ninyi pa kwenda. Namba za siri ni .......” Mzee Gomez akataja tarakimu nne za kufungulia mkoba wake.

    “Usimuache mwanangu, tafadhali Peter. Tokeni haraka humo ndani. Vanee anajua njia, kimbieni mbali na hapo kuna wajinga wanat .........” Mzee Gomez hakumaliza sentensi yake simu ikawa imekatika.

    Haraka Peter akanyanyuka na kwenda chumbani kwake na kuchukua baadhi ya nguo. Kisha akamfuata Vanessa ambaye alikuwa chumbani kwake naye akipanga nguo kidogo kwenye begi lake.



    Peter akachukua mkoba alioambiwa na Mzee Gomez, kisha akamkamata Vanessa mkono na wakati huo begi lake la nguo lilikuwa mgongoni.

    “Ni wapi tunapitia?” Peter alimuuliza Vanessa baada ya kutoka mle chumbani kwake.

    Vanessa huku akipachika begi lake mgongoni, akatamgulia mbele na kwenda chumba kimoja ambacho walikuwa wanatumia kama stoo. Wakaingia na bila kuchelewa, Vanessa alitoa baadhi ya vitu ukutani. Hapo zikaonekana namba ambazo Vanessa alizibofya na mara ukuta wa stoo ile ukafunguka.

    Ulipofunguka ukuta ule, taa zikaanza kuwaka na kuangaza ndani mwote ambapo walipaswa kwenda vijana wale wawili.

    Mzee Gomez alitengeneza handaki kwenye nyumba yake. Peter akabaki mdomo wazi asiamini kile alichokuwa akikiona. Vanessa akawa wa kwanza kuingia ndani ya handaki lile, na Peter alifuatia na hapohapo mlango ule wa ukuta ukafunga.



    Safari ya kwenda pasipojulikana ikaanza huku Vanessa akiwa mstari wa mbele kuongoza msafara ule. Hadi muda huo Peter alikuwa bado haamini anachokiona. Alikuwa anatamani kumuuliza Vanessa, lakini kwa wakati huo binti alikuwa katika harakati za kufuata njia inayowapeleka nje.

    Baada ya dakika zisizozidi kumi, mara wakasikia milipuko ya bunduki kule walipotoka. Hapo Vanessa alijisemea mwenyewe kuwa kazi imeanza.

    Milipuko hiyo ilikuwa inatokea nyumbani kwao, na mapigano yalikuwa ni kati ya walinzi na wavamizi wa nyumba ya Mzee Gomez. Hivyo Vanessa baada ya kusikia, alijua kabisa hakuna kitakachosalia katika nyumba yao. Na huko wanapoelekea ndipo hasa palimfanya aseme kazi imeanza.



    Wakazidi kuliandama lile handaki refu, linaloweza kupitisha hata magari madogo kama tax. Na hakika lilikuwa refu hasa, kwani baada ya dakika arobaini na tano, ndipo Peter na Vanessa walijikuta wapo nje.

    Walipoangalia nyuma ilipokuwa nyumba yao, waliona wameiacha mbali sana. Na bila moto ambao ulikuwa unawaka kwenye nyumba yao, sidhani kama wangeiona. Kwa kifupi, katika mapigano yale ya walinzi na wavamizi, wale wavamizi ndio walioshinda mapigano.

    Baada ya kushinda, waliingia ndani na kuanza kuwatafuta Peter ambaye kitambo sana alikuwa anasakwa, na pia Vanessa ambaye baba yake ndio kamuingiza kwenye kutafutwa huko.

    Wavamizi walipowakosa, waliamua kuichoma moto nyumba ile kubwa na kisha wakatitia yalipomakao yao. Huo ndio ukawa mwisho wa jumba kubwa la Mzee Gomez.

    Vanessa akatema mate pembeni, kisha akatoa chupa ya maji, akanywa. Akamtaka Peter ampe ule mkoba wa baba yake. Naye Peter bila kinyongo, akampa na kumuangalia anachotaka kufanya.



    Vanessa akaanza kuhangaika kubonyeza namba zilizopo kwenye mkoba ule ili aweze kuufungua. Peter kuona hivyo, akaamu kumsaidia kuifungua kwa namba za siri alizopewa na Mzee Gomez.

    Mkoba ukafunguka na Peter akasogea pembeni ili kumpa uhuru Vanessa kupekua vitu vya mzazi wake ambaye aliviweka kuwa siri yake na ndio maana aliwasihi sana waondoke na mkoba huo na si kingine.

    Vanessa akaanza kupangua baadhi ya vitu vilivyomo humo ambavyo vingi vilikuwa ni makaratasi. Pia kulikuwa na bastola moja na boksi dogo lililojaa risasi. Muda huo ilikuwa ni saa tatu za usiku.

    “Pity. Njoo hapa.” Vanessa alimuita Peter mahala ambapo yeye alikuwa amechutama na kurunzi yake akipekua vilivyomo kwenye mkoba wa baba yake.

    Peter akasogea kama alivyoambiwa, lakini alishtuka sana kukutana na bastola ikiwa imekandamiza makaratasi yaliyokuwa pembeni.

    Vanessa hakujali hali hiyo wala kufikiria chochote kuhusu Peter. Yeye alichofanya ni kumpa maelezo anayotakiwa kuyafuata kwa usiku ule.



    “Hii hapa ni ramani,” Vanessa alimuonesha Peter ramani aliyokuwa kaitandaza juu ya mkoba ule. “Sasa hivi tupo hapa, na tunatakiwa twende hapa. Panaitwa BORN TO DIE Camp. Hii ndio kambi kubwa ya waasi wa nchi hii. Baba anamahusiano nao mazuri, hivyo kwa msaada wako wa kusoma ramani, naomba twende hapa. Tutakuwa salama zaidi.” Vanessa alimwambia Peter huku akiikunja ile ramani ndogo na kumapatia Peter.

    “Hii hapa ni dira na silaha yako.” Vanessa akampa kisu Peter ambacho katika mpini wake kulikuwa na dira inayotoa mwanga kwa usiku ule. Peter akapokea, na hapo Vanessa akafunga ule mkoba wa alioachiwa na baba yake.

    Akasimama wima na kuipachika bastola yake nyuma ya mgongo na kuibana kwa kutumia kiuno cha suruali ya jinzi aliyokuwa kaivaa.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Peter bado alikuwa hana cha kusema na mwenye wingi wa maswali kwa kile ambacho alikuwa anakiona kwa wakati ule.

    “Vanee. Mbona huogopi hiyo siraha?” Peter alimuuliza Vanessa.

    “Natakiwa kutoigopa kwani kwa sasa endapo utaigopa, utakuwa unajiua mwenyewe. Ni heri hii iwe msaada kwangu kuliko kuwa sina kitu.” Vanessa akamjibu Peter huku akimpita pale alipokuwa kasimama.

    Vanessa akaanza kuongoza njia ambayo kiasi fulani alikuwa anaifahamu.



    “Na baba yako. Kawajuaje hawa Waasi?” Swali lingine kutoka kwa Peter kwenda kwa Vanessa.

    “Licha ya baba kuwa anachukua maliasili za Afrika na kuzipeleka mabara ya nje, pia alikuwa anachukua silaha na kuziingiza barani Afrika. Na zaidi alikuwa anawapa Waasi. Hivyo wanamfahamu kwa njia hiyo. Na hauzi silaha hapa Senegal tu. Kongo kauza sana, Nigeria kawauzia pia Sudan, Rwanda na Burundi, kwote huko kafanya kazi na wanamjua vyema.” Vanessa alimjibu huku akianza kuingia katika msitu mmoja mnene na wa kutisha kwa kuuangalia kwa nje.





    “Kwa nini hukuniambia haya mapema?” Peter alilalamika.



    “Ungekimbia na wakati nilikuwa nakuhitaji sana katika kufariji maisha na hisia zangu.” Jibu lilitoka bila Peter kuangaliwa usoni.



    “Hatari sana hii. Maisha yameingia doa haya.” Peter aliongea kwa sauti ya kukata tamaa.



    “No Pity. Kuna muda yakupasa kuelewa maisha ni aina ya fumbo gumu kulifumbua. Kulifumbua kwake ni wewe kujielewa unatakiwa kufanya nini. Kile kitu ambacho unakufa unakifanya, ndicho kinachotambulisha maisha yako.

    Kwa hiyo, fumbo la maisha yako ufumbuka pale moyo wako unapokubaliana na ufanyacho. Hivyo, kwa sasa wewe hujui maisha yako yapo vipi, yawezekana huku uendapo ndipo maisha yako yanapaswa kuwa. Yawezekana kabisa, huku ndipo MUNGU alipokupangia kuwe ndio maisha yako. Usiseme yameingia doa.” Maneno mazuri yalitoka kwa Vanessa.



    “Kwa hiyo wataka kusema mimi nimepangiwa kuwa Muasi?” Peter aliuliza swali lingine na kumfanya Vanessa asimame na kumgeukia kijana yule wa kiume.



    “Hujui chochote Pity. Hujui ni kwa nini hawa Waasi wapo katika nchi hii. Hujui hata kidogo na kamwe hutojua hadi pale utakapotambua kuwa unadhurumiwa hata haki yako ya kuishi. Tunasikia wangapi wanakufa kila kukicha katika nchi hii? Nani anayefanya yote haya? Nani aliyeteketeza familia yako? Ni nani ambaye ulimuamini na akaja kukusaliti?” Vanessa aliuliza maswali mfululizo na hakutaka kumpa nafasi Peter ya kujibu maswali hayo. Akaendelea,



    “Ni hao mnaowaita Wanasiasa. Hao mnaowaweka madarakani wale keki ya nchi hii. Wajilimbikizie makontena ya fedha vyumbani mwao. Walale juu madini yetu. Wavae mawani zenye nakshi za dhahabu pamoja na mavazi yaliyopambwa na vifungo vya meno ya wanyama wetu huku uturi mwanana wa gesi zetu ukiwafanya wanukie raha kuliko shida.” Hisia kali zilikuwa zimemtawala Vanessa wakati anaongea haya, na hakika alikuwa anaijua Serikali yake.



    “Huwezi jua haya Pity. Najua unashikwa na kicheko sana pale wale uliowachagua wanapokuwa wamesinzia bungeni. Lakini pale unapoangalia kiundani, yule ni mnyanyoji. Yeye kalala ndani ya bunge na anachukua msharaha kama kawaida. Lakini tupo tunaokesha macho kodo tukitafuta japo senti na hatuipati. Chukulia mfano hawa wachimba madini, wanaweza kukaa chini ya ardhi hata wiki moja wakisaka madini. Hawalali wala kujisikia kulala kwao hakupo. Na wanaweza wasipate chochote.

    Lakini kuna wajinga wanalala kazini, na wanaingiza kiasi kikubwa cha fedha kwa siku. Huo si unyonyaji? Nini unawasaidia wananchi wako kama kazi yako kulala kazini?



    Wake up Pity. Amka Peter. Kuna watu wanaona haya na wanataka wayakomeshe. Ni lazima nchi na dunia kwa ujumla ielewe maumivu yetu. Si mbaya tukionekana tupo kinyume na serikali, lakini tunafanya kile tunachoona kipo sahihi.” Vanessa alimaliza kuongea na kuzama ndani ya msitu akimuacha Peter kwenye ukiwa wa kifikra.



    Maneno yalimuingia Peter na akaona ni heri akajaribu kuanza maisha ya kiasi kuliko kuendelea kunyonywa na serikali ambayo haijadili maisha ya masikini bali wanajadili kuhusu fedha pekee.

    *****

    Safari katika msitu ule mkubwa ilikuwa inaendelea kimyakimya huku ni nyayo na wadudu wa usiku ndio walikuwa wanatoa sauti usiku ule.

    Masomo ambayo Peter aliyasoma alipofika kwa Mzee Gomez, ndiyo yalikuwa yanasaidia katika kuisoma ramani na dira aliyokuwa nayo.



    Walitembea umbali mrefu sana kwa usiku ule. Hadi saa tisa za usiku, bado walikuwa wanaitafuta kambi kuu ya Waasi wa nchi ile ya Senegal.

    Ikabidi wapumzike kwa muda wa saa moja kabla hawajachukua masaa mawili mengine kuitafuta kambi hiyo.

    *****

    Ilikuwa ni kambi moja kubwa sana ambayo ilijengwa mahala ambapo si rahisi kwa watu wasiopajua kufika. Ilikuwa imejikamilisha kwa kila kitu. Muda ule wa saa kumi na mbili alfajiri ambao Vanessa na Peter walikuwa wamefika, waliweza kushuhudia wanajeshi wakifanya mazoezi ya viungo na wengine kukimbia mchakamchaka.

    Pia kulikuwa kuna magari mengine ya jeshi yanaingia huku yamebeba majeruhi ambao walikuwa wamevaa kiraia na wengine kijeshi.



    Walipoingia kambini mle, kuna baadhi ya wanajeshi waliwaoneshea mitutu ya bunduki huku wanajeshi hao wakiwataka watoe silaha zao na kuwakabidhi.

    Peter akiwa anatetemeka, alitoa kisu chake na kukirusha mbele ya wanajeshi wale kisha akanyoosha mikono juu.

    Vanessa naye alitoa bastola yake pamoja na mkoba wa baba yake, kisha akavitupia mbele yao na kufanya kama kile alichofanya Peter, kunyoosha mikono juu.

    Mwanajeshi mmoja aliokota silaha zile na mkoba, na mwingine alienda nyuma ya akina Peter na kuwavua yale mabegi yao waliyobeba nguo. Peter na Vanessa, wakaamuriwa waanze kwenda ndani ya kambi ile.



    Ilikuwa kama bahati, kwani kabla hawajaingizwa ndani zaidi ya kambi ile, alitokea mwanajeshi mmoja ambaye alikuwa anacheo kuliko wale waliokuwa wamewaweka chini ya ulinzi.



    “Hey. Waacheni hao. Waleteni huku.” Sauti ilisikika nyuma ya wale wanajeshi waliokuwa wamewateka wakina Peter.

    Waligeuka nyuma na walipoona ni mkubwa wao, walitii amri na kuanza kwenda nao pale alipokuwepo yule mkuu.



    “Hawa ni mali ya Mzee Gomez. Alitoa taarifa jana tuwapokee.” Yule mwanajeshi mwenye cheo alitawatambulisha wale wanajeshi wenzake wadogo.



    “Okay. Samahani sana jamani.” Wanajeshi waliomba radhi kwa akina Vanessa na kisha kuwakabidhi vitu vyao.

    Yule mkuu zaidi ya wale wanajeshi, aliwachukua wakina Peter na kuwapeleka vyumba vya kupumzikia kwani alijua walikuwa wamechoka sana.



    Peter na Vanessa wakawekwa kwenye vyumba tofauti ili wapumzike. Ndipo wakati huo Vanessa alipata fursa nzuri ya kusoma makaratasi aliyoachiwa na baba yake, Mzee Gomez. Yalikuwa ni makaratasi mengi, lakini moja ndilo lilikuwa la muhimu sana kwa binti yule.

    Karatasi hilo lilikuwa limeandikwa wosia mrefu ambao Vanessa alipata kuusoma na kuuelewa vizuri sana. Kitu cha maana ambacho Vanessa alikiona kwenye wosia ule wa baba yake, ni kuhusu uhusiano wake na Peter.



    “Najua wewe ni mtoto wangu, lakini kwa wengine we si mtoto wao na wala si mtoto kabisa. U mtu mzima na unayejitambua. Uhusiano wako na Peter, nategemea ufike mbali sana. Nimempenda huyo kijana kama ulivyompenda wewe. Ni kijana jasiri sana, ni kijana ambaye ukimkumbatia kwa imani na tumaini, hakika mtafika mbali sana. Bado ni mchanga katika nyanja hizi za mapigano na maisha ya kuhama-hama. Nategemea siku moja awe kama wewe. Na huyo akiwa kama wewe, amini nakwambia Vanee, ndiye atakuwa msingi imara wa maisha ya kambi ya waasi ya huku Senegal. Nenda naye, na mfanye awe na ujasiri wa kutumia ujasiri wake. Naamini mtafika mbali.” Huo ni ujumbe ambao aliuacha Mzee Gomez kwenye wosia wake mrefu kwenda kwa binti yake.

    Baada ya kumaliza kuusoma wosia ule, Vanessa aliukunja vizuri na kuuhifadhi kwenye ule mkoba wa baba yake na kisha akakaa kitandani na kuanza kufikiria mambo ambayo yanaweza kuwa yamempata baba yake.

    Alifikiria mengi sana, lakini hayo mengi yalikuwa hayana mwisho zaidi ya kupitiwa na usingizi mzito uliotokana na mchoko wa safari ndefu

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    ****



    Baada ya usingizi mrefu, Peter alinyanyuka toka kitandani alipokuwa amelala na kutoka nje. Ulikuwa ni muda wa jioni ambapo pale kambini wanajeshi walikuwa wanamalizia mazoezi na watoto walikuwa wanacheza kwa furaha hapo nje.

    Peter alichukua nafasi sehemu moja na kukaa, kisha akaanza kuwaangalia watoto wale walivyokuwa wanacheza.

    Katika watoto wote waliokuwa wanacheza, alivutiwa na watoto wawili ambao mmoja alikuwa wa kiume na mwingine wa kike. Yule wa kiume alikuwa mkubwa kiasi kuliko yule wa kike.

    Watoto wale walikuwa wanacheza mchezo maarufu kwa watoto, uitwao ‘BYE SHOW’. Jinsi walivyokuwa wanacheza, Peter alijikuta anadondosha machozi.

    Ni mchezo ambao alikuwa anapenda sana kuucheza na mdogo wake wa kike enzi za uhai wake. Mchezo ambao Christina alikuwa hajisikii raha siku nzima kama hatoucheza na kaka yake kipenzi, Peter Madira. Leo mchezo ule anashuhudia ni watoto wengine ndio wanaoucheza, hakika ilikuwa inamuuma sana na kutoa machozi ilikuwa ni halali yake.



    “Kuna muda unatakiwa kusahau kumbukumbu zinazoweza kukutoa machozi. Yaliyopita, yamepita. Achana nayo na ishi na haya yanayokuzunguka, ishi maisha ya sasa. Yaliyopita yawe muongozo tu kwako ili usije kurudia pale ulipokosea.” Maneno hayo yalikuwa yanaingia vizuri masikioni mwa Peter na alipoangalia ni nani anayemwambia hayo, alikuta ni Vanessa.

    Vanessa naye alikuwa katoka kupumzika, na ndipo alipotoka nje na kumkuta Peter akiwa kakaa peke yake huku akiwa katika kumbukumbu zilizokuwa zinamtoa machozi. Alipoangalia ni wapi palipompeleka katika kumbukumbu hizo, alikuta ni kwa wale watoto wawili. Hapo ndipo alichukua jukumu la kumwambia maneno yale.

    “Hakuna anayeishi bila kumbukumbu za nyuma Vanee. Kila mtu anategemea kumbukumbu ili aishi. Kama huna kumbukumbu, maisha yako yatakuwa na mashaka sana katika hii dunia. Nimeikumbuka familia yangu, na nimekumbuka maisha ya nyumbani enzi zile. Furaha tuliyokuwa nayo, imetoweka ghafla, ni kama vumbi litimkalo kwenye kiyoyozi.



    Huwa kubwa sana wakati linatimka, lakini halidumu kwa kuwa kiyoyozi hulimeza vumbi hilo haraka sana.” Peter aliongea maneno hayo huku akiwa kaelekeza macho yake kwa watoto wale wawili.

    “Kwa sasa, sina mahala tena pa kuipata furaha ile ya zamani. Furaha ya kumbate la wazazi na ndugu. Lazima nidondoshe machozi kila napogundua hili. Hakuna ajuaye maumivu yangu kama hajawahi kupatwa na nilichopatwa mimi, hakuna ajuaye kama hajui maumivu ya kuchukuliwa wazazi na ndugu zake wote. Familia yangu imenyang’anywa maisha yao na watu wachache wenye uchu wa kuimiliki dunia peke yao. Inaniuma sana Vanee.” Peter aliongea huku bado macho yake kaelekeza kwa wale watoto.

    Vanessa badala ya kuongea au kumshauri chochote Peter, hakufanya hivyo na badala yake alimrushia gazeti Peter na Peter akalichukua na kuanza kuliangaza.

    Ukurasa wa mbele kabisa ulikuwa na kichwa cha habari kilichokolezwa maandishi yake.



    Kilielezea mauaji ya kutisha ya Bwana Gomez, baba mzazi wa Vanessa. Ilikuwa ni taarifa iliyomshtua Peter kiasi kwamba alishindwa kuendelea kulisoma lile gazeti na kumuangalia Vanessa yupo katika hali gani.

    Jibu alilolipata kwenye uso wa Vanessa, alishindwa kumtafasiri mwanadada yule. Alikuwa mkavu wa sura na asiyeonesha kuumizwa na ile taarifa.

    Peter akarudisha macho yake katika lile gazeti na kuanza kulisoma kwa makini. Habari zilisema Mzee Gomez ni haramia anayehujumu nchi kwa kuwauzia silaha waasi mbalimbali wa Barani Afrika. Habari haikuishia hapo, ikaenda hadi kwa watu aliokuwa anaishi nao Mzee Gomez, ambaye ni Peter na Vanessa. Dau likawekwa kwa atakayewapata wakiwa hai au wafu, watapewa kiasi kikubwa cha fedha.



    Msemaji mkuu wa hayo yote alikuwa ni Mkuu wa Polisi wa nchini Senegal kwa niaba ya Waziri wa Ulinzi wa nchi ile.

    Peter akashusha pumzi ndefu na kumuangalia Vanessa aliyekuwa kasimama hatua chache pembeni yake huku mikono yake kaikunjia kifuani.

    “Wakati mtoto anapozaliwa, asipolia basi mama na wauguzi hushikwa na mashaka sana. Hufanya kila njia ili mtoto huyo atoke sauti ya kilio. Na pale wanapofanikiwa kumliza mwana huyo, basi vicheko na nyuso za furaha huwakumba.

    Lakini ukishakuwa mtu mzima, mwenye kujielewa kwa kile ukifanyacho. Ukiwa kimya, yaani wewe unafanya yako tu. Hakuna ambaye atakuja kukufanya chochote. Ila ukiwa unalia, ni lazima watakuja kukuuliza kuna nini.



    Hyo ni tofauti kati ya mtoto na mtu mzima. Kwa mtoto akilia, ni furaha ya mama. Ila mtu mzima akilia, ni lazima tuulize kuna nini?

    Lakini ni vipi ukiona jambo linaloweza kukuliza halafu mhusika aliyetokewa na jambo hilo halii?” Vanessa alikuwa anaongea hayo huku bado kasimama. Akaendelea,

    “Kulia si suluhisho la matatizo. Na kulia hakurudishi ukweli uliotokea. Namaanisha, mimi kumlilia baba yangu, haitosaidia kumrudisha duniani tena. Nauchungu wa kumpoteza, ila moyo ndio unaolia. Moyo ndio unaoelewa machozi niyatoayo kwa baba yangu.” Vanessa aliongea huku machozi yakianza kumrenga-renga lakini alijikaza ili yasidondoke.

    “Pity, unatakiwa kuwa jasiri kwa sasa. Hayo mambo ya kulia-lia, tuwaachie watoto wachanga. Sisi ni watu wazima tunaoelewa nini cha kufanya. Tusimame imara ili kupambana kwa sasa, hapa tulipo ndipo pa kuanzia,” Vanessa alimaliza kuongea lakini Peter hakuafiki maneno ya mwisho aliyoyaongea Vanessa.



    “Unataka na mimi nishike bunduki ili niingie vitani, si ndio maana yake au? Ha ha haaa, Vanessa you are out of your mind. (Hujielewi)” Peter alimwambia Vanessa ni kama kichaa kwa yale anayofikiria.

    “Tatizo lako hufahamu nini ambacho yapaswa ufanye. Na hutofahamu hadi pale utakapofungua macho yako ‘kodo’. Hapo ndipo utaelewa nini yakupasa kufanya. You are a soldier Pity, believe me. We are the soldiers,” Vanessa aliongea huku anachutama na kushika mikono ya Peter.

    “Okay.” Peter alimjibu kifupi Vanessa kwani alijua akiendelea kubishana kuhusu hilo, hata mapenzi yao yanaweza yakaingia doa.

    Vanessa akakaa pembeni ya kijana yule na kulaza kichwa chake kwenye bega la kushoto na yeye macho akayaelekeza kwa wale watoto wanaocheza ‘BYE SHOW’ na Ester.



    “Kesho mkuu wa jeshi anakuja,” Vanessa aliongea hayo baada ya kimya cha dakika kama kumi.

    “Mkuu wa jeshi gani. Wa nchi hii?” Peter alisaili.

    “Hapana. Mkuu wa kambi hii. Aliyeanzisha hii kambi ya waasi.” Vanessa alimfafanulia kijana yule.

    “Okay. Kwa hiyo,” Peter alitaka kujua zaidi.

    “Kengele ikigongwa asubuhi, yatupasa kutoka na kukaa mstarini kwa ajili ya kusikiliza mawaidha yake.” Vanessa aliendelea kutoa maelezo kwa yale anayotakiwa kuyajua Peter.

    “Okay. Hamna tatizo.”

    Baada ya maneno hayo waliendelea kuongea mangine hadi pale muda wa kuingia ndani ulipowadia.



    Ilikuwa ni asubuhi moja tulivu kabisa kupata kutokea katika kambi ile. Kulikuwa hakuna ngurumo za gari wala ndege za kivita bali ni sauti ya upepo na viumbe wa angani ndio walikuwa wanashangwesha nchi ile ya Waasi.

    Wakati hayo yakiendelea kuchukua nafasi huko nje, huku ndani Vanessa na Peter walikuwa wamekumbatiana wakiwa katika usingizi mzito kutokana na mahaba waliyoshinda wanapeana usiku uliopita.

    Usingizi wao ulikuja kukatika baada ya kengele ya dharula kugongwa kambini pale. Kengele hiyo ilikuwa inamengi ikigongwa, hivyo wananchi wa kambi ile walipoisikia, walinyayuka haraka na kwenda kusikiliza ni nini kilichokuwa kinatokea.



    Vanessa na Peter walikuwa wanajua ni nini kinachoendelea, walivaa mavazi yao na kisha wakatoka nje ambapo walikuta watoto na mama zao wakirudishwa ndani na pale nje wakabaki vijana pamoja na wanajeshi wakiwa wamesimama katika mistari mnyoofu.

    Peter na Vanessa nao waajiunga katika mistari hiyo na kusubiri kuona kinachofuata.

    Hapo alitokea mwanajeshi mmoja mweusi na aliyeenda hewani akiwa kavaa gwanda za mabaka ya kijani na meusi kwa mbali kama zile gwanda za wanajeshi wa Cuba.

    “My name is Commender Bonito Muchakila. You can call me Commender Bonito. ( Jina langu ni Kamanda Bonito Muchakila. (Unaweza kuniita Kamanda Bonito).” Aliongea jamaa yule kwa lafudhi kama ya Kikongo. Akaendelea kujieleza kwa lugha ya Kiingereza (Nimeitafsiri).



    “Ukiwa hapa, tayari we' ni mwanajeshi. Mwanajeshi anaishi kwa sheria anazozikuta na zitakazokuja,” Kamanda Bonito alikuwa akiongea huku kaweka mikono yake nyuma, na ile kofia yake ya kijeshi na vyeo vilivyotapakaa mabegani kwake, huku kiunoni akiwa kaweka pochi yenye bastola, ni nani ambaye angethubutu kuongea.

    “A coward dies a million of deaths. A soldier dies, but die once. (Muoga hufa vifo milioni. Mwanajeshi anakufa, lakini hufa mara moja).” Kamanda Bonito aliongea hayo maneno.

    “Tupac (2 Pac) said that. (Tupac alisema hayo).” Alimaliza kwa kusema hiyo kauli ya muoga, Tupac ndiye aliyewahi kuitamka.

    Baada ya maneno hayo, mara akatolewa kijana mmoja aliyekuwa kafungwa mikono kwa nyuma na kuletwa pale mstarini na kupigishwa magoti akiwa katika uoga mkubwa na uso wake umechakaa kwa vidonda pamoja na damu.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Huyu ni muoga,” Kamanda Bonito aliongea huku akichomoa bastola yake kiunoni na kuifyatua ambapo risasi zile zilitua vizuri kwenye miguu ya kijana yule.

    “Na muoga hufa vifo zaidi ya milioni,” Akamfata pale alipo yule jamaa aliyekuwa analia kwa nguvu kutokana na zile risasi kumuingia.

    Kamanda Bonito akampiga teke la kidevu na kumfanya yule jamaa arushe udenda uliojaa damu na huku akipinduka kinyume kwa kurushwa juu na teke lile, ungemuona ungesema labda ni kuku ndiye aliyepigwa peke hilo jinsi alivyopaa. Kamanda Bonito hakuishia hapo, alimfata na kuzidi kumshushia kipondo cha haja jamaa yule.

    “Na utakufa, na kufa, na kufa. Na kufa.” Aliongea hayo huku akimshushia kitako cha bastola usoni jamaa yule aliyekuwa hajielewi tena tangu ale teke lile kali la kidevu.



    “This is how a coward dies (Hivi ndivyo mwoga hufa).” Aliongea Kamanda Bonito huku akinyanyuka pale alipokuwa kamkalia yule jamaa.

    Yule jamaa akiwa hajitambui, yupo kwenye mawenge yasioelezeka, naye alianza kujizoa-zoa pale chini taratibu na mwisho wake alinyanyuka na kupiga magoti huku akiwa kainama na damu kuchuruzika kama jasho toka pembeni ya uso wake uliokuwa umebadilika na kuwa wenye vidonda na vimbe nyingi.

    “Na zaidi ya yote, mwoga hufa kama hivi.....” Kamanda Bonito alinyoosha mkono wake wenye bastola na kulenga kichwa cha yule jamaa. Kisha akaanza kubonyeza kifyatulio cha bastola ile kwa ajili ya kumuua kabisa yule jamaa.

    Akiwa kabakiza sekunde kama moja kwa ajili ya kutimiza azma yake, mara mkono wake ulipigwa kwenda juu na kuifanya ile risasi kufyatulikia juu. Hapo Kamanda Bonito aling’aka kwa hasira na wakati huo wanajeshi wengine wakiguna kwa hamaniko kwa kile kilichotokea.



    “Unafanya nini mshenzi wewe.” Kamanda Bonito alifoka huku akimfata yule aliyesababisha zoezi lake la kuua.

    “Hatupo hapa kuoneshana ubabe wala kuuana wenyewe kwa wenyewe. Tupo hapa kwa ajili ya kutetea haki za watu wanaougua na serikali yetu. Watu ambao wanalia kila kukicha kwa sababu ya vita vyetu. Watu wanaopoteza mamia ya makazi na watoto kwa sababu yenu nyinyi na serikali.

    Watoto kila leo wanapoteza wazazi na ndugu, wanapoteza matumaini ya kuishi kama binadamu anavyopaswa kuishi. Tuwapeleke wapi kama hata huku wanapoona panafaa kukimbilia napo kuna mauaji ya mkuu na wanajeshi wake? Tukimbilie wapi sisi waoga? Na tutakimbia wangapi na mpaka lini?” Kamanda Bonito alijikuta amesimama bila kupiga hatua yoyote wakati kijana mpya wa kambi ile akiongea hayo.

    Alikuwa ni Peter Madira. Muathirika wa serikali iliyokuwa madarakani. Alikuwa kakerwa na ile tabia ya Kamanda Bonito kumpa kipigo yule jamaa aliyekuwa bado anayasikilizia maumivu makali yaliyotokana na kipigo cha mkuu wake. Peter aliendelea,



    “Tunatakiwa kujiunga na kuwa kitu kimoja. Kumuua muoga haimaanishi umeshinda mapambano ambayo yanakukabili. Kumuua muoga hakujengi ujasiri kwa wale walioshuhudia mauaji, na badala yake huongeza uoga kwa kundi lako na kazi huwa mbovu. Mtu atafanya kazi kwa kujishtukia, anajua akikosea tu, bosi wake atamuadhibu. Hivyo atafanya kazi akitetemeka na mwisho wake huaribu.

    Je? Utaua wangapi kwa sababu ya woga wao? Na zaidi ya hiyo, unadhani utampata nani ambaye atalia pale utakapodondoka? Unadhani wangapi hadi sasa wapo tayari kukukimbia kwa sababu ya ukatili wako?

    Amka mkuu, huu si uwanja wa kuwajaza watu ujasiri kwa kuua waoga. Huu ni uwanja wa kuongeza majasiri kwa maneno ya kuwainua na kuwajenga. Hakuna aliyekuja hapa kupoteza uhai wake, hawa wote wamekuja kwa kuwa walijua hapa kuna usalama.

    Kama kuna usalama huu, ni bora warudi walipotoka na kufia huko kwenye majumba waliyoachiwa na wazazi wao kuliko kufia hapa tena kwa kosa ambalo ndilo limemtoa kwao.



    Wote tumekimbia kwa sababu ya kuogopa. Hata wewe umejificha kwa kuwa unaogopa. Je, nawe ufe?” Peter alimaliza kuongea kwa kumuuliza swali Kamanda Bonito ambaye alikuwa kimya wakati hayo yanaongewa.

    Kamanda Bonito alikaa kimya na kumfanya Peter amalize kabisa maneno yake.

    “When time comes, we will die. But not like that. (Muda utakapofika, tutakufa. Lakini si kama vile). Unamuua wakati anahitajika, that’s unfair.” Peter safari hii aliongea kwa uchungu na kuamua kumpa mgongo Kamanda Bonito na kilichofata hapo ni Peter kuondoka pale mstarini.

    Kamanda Bonito alishusha pumzi ndefu huku akiwa kama haamini kile alichokuwa kakisikia. Ama hakika maneno yale yalimuingia kisawa –sawa.

    Alimuangalia yule jamaa aliyekuwa kajiinamia pale mbele ya umati wa watu. Kisha kwa mkono wake alinyoosha bastola yake na kuifyatua ambapo risasi kadhaa ziliingia kichwani kwa jamaa yule na kuchukua maisha yake.



    “When time comes, we will die. We all die. But some, they will die when are sleeping, and others will die by swords. But a soldier, dies by a gun only. (Muda utakapofika, tutakufa. Wote tutakufa. Lakini wengine watakufa wakiwa wamelala, na wengine kwa upanga. Ila mwanajeshi, hufa kwa bunduki tu.” Kamanda Bonito aliongea huku akiipachika bastola yake kiunoni.

    “No. Only true soldiers will die by a gun. He is a true soldier. (Hapana. Ni wanajeshi wa ukweli ndiyo watakaokufa kwa bunduki. Huyu ni mwanajeshi wa kweli).” Kamanda Bonito alimaliza kwa kuipigia saluti maiti ya yule jamaa na kisha akatoka pale mstarini na kwenda zilipo ofisi za kambi ile.



    *****



    “Kamuua yule mwanajeshi,” Vanessa alimwambia Peter ambaye alikuwa kasimama kwenye kichuguu kimoja pale kambini na macho yake akiwa kayaelekeza kwenye pori nene lililokuwa limezunguka kambi ile.

    “A real soldier, finish what he starts. (Mwanajeshi wa kweli, humaliza kile alichokianza).” Peter alijibu na kuendelea kuangalia kule mbali ulipo-msitu.

    “Alitakiwa kufanya hivyo. Na kila mwanajeshi anaelewa hilo. Na mwisho wake huwa ni yeye kuukubali ukweli kwa kile alichokifanya.” Peter alizidi kumfungua Vanessa.



    “Haya umeyajuaje Peter.” Vanessa aliuliza kwa mshangao.

    “Kuna muda unatakiwa kusoma hata yale ambayo huna uhakika kama yatakuja kukusaidia. Nilikuwa nasoma na kuangalia filamu za kivita kila nilipopata muda. Nilikuwa napenda sana kujifunza mambo yao. Huko ndipo nilipojifunza.” Peter alijibu.

    “Hiyo nzuri sana. Na pale ulifanya jambo la kijasiri sana kumwambia yale yote Kamanda.” Vanessa alipongeza.

    “Yapasa kusimama kwenye ukweli ili kuokoa nafsi zinazokuja kuhangamia. Bila kusema ukweli, wote tutahangamia kwa sababu ya matendo au hali tuliyozaliwa nayo. Nitasimama kwenye ukweli hadi pale nitakapokufa.” Peter aliongea huku akizidi kukazia macho kule alipokuwa anaangalia tangu mwanzo.



    “Lakini angalia usii...” Vanessa hakumaliza maneno aliyokuwa kadhamiria kuyaongea, mwanajeshi mmoja alikuja na kumuita Peter kwa kumwambia kuwa anaitwa na mkuu, yaani Kamanda Bonito.

    “Nakuja.” Peter alimwambia mwanajeshi yule na kuendelea kusimama pale kwa dakika kadhaa nyingine kabla ya Vanessa kuanza kumsihi aende kwa Kamanda bonito haraka.

    Peter alimsikiliza mpenzi wake na bila kupoteza muda alishuka toka pale kwenye kichuguu na kuelekea kule alipokuwa anaitwa.

    “Watu wengi huogopa kusema ukweli kwa kile ambacho wanadhani wakisema watadhurika. Lakini ukweli ni kwamba, hakuna binadamu ambaye hafanyi makosa wala hakuna binadamu anayejitambua awezaye kuukataa ukweli. Kifupi hakuna binadamu aliyekamilika.” Aliongea Kamanda Bonito huku akiwa anaangalia dirishani na wakati huo Peter alikuwa nyuma yake kakaa kwenye kiti kimojawapo mle ofisini. Kamanda Bonito hakuishia hapo.



    “Uoga upo kijana, lakini si uoga wa kufanya lililosahihi hasa kwa mwanajeshi aliyekamilika kama mimi. Siwezi nikajiita mwanajeshi wakati naogopa kufyatua risasi au kutumwa sehemu yenye mapambano. Huo ni uoga wa kijinga, na yeyote mwenye uoga wa namna hiyo, anatakiwa auawe. Hivyo ndivyo sheria isemavyo hapa.

    Lakini umeongea kitu cha msingi sana Peter.” Kamanda Bonito sasa alimgeukia Peter na kumuangalia usoni.

    “Nitaua na kuendelea kuua wangapi kama wote wakiwa hivi? Wangapi watakufa kwa risasi yangu? Wangapi watapona kama nikiendekeza kuruhusu risasi yangu itoke kwenye kinywa cha bunduki yangu? Kifupi ni wengi sana hawatapona.” Kamanda aliongea huku akitikisa kichwa kushoto kulia kwa masikitiko.



    “Njia pekee ya hawa watu kuutoa huu uoga ni kuwapa mafunzo halisi ya kijeshi. Mimi ni mwanajeshi halisi, najua cha kufanya. Hata kama wewe si muoga, kama ulivoonesha pale, ni lazima upite katika mafunzo hayo. Na ukipita hapo u mzima, hakika wewe utakuwa imara katika maamuzi yako.

    Hawa uaonao, walikuja kwa mapenzi ya vita na wegine kwa visasi vya familia zao. Na sisi kwa kuwa tunahitaji jeshi, tuliwapa bunduki bila mafunzo ya kijeshi bali jinsi ya kuitumia bunduki hiyo. Matokeo yake sasa wakienda huko hufa hovyo kama kuku wenye mdondo.” Peter alikuwa akimsikiliza Bonito kwa makini bila kuongeza chochote.

    “Mafunzo haya yataanza wiki ijayo. Sitapeleka tena jeshi kupigana kwa sasa hadi baada ya mafunzo hayo kuisha. Hii ndio kambi ya BORN TO DIE, lazima iendane na neno hilo.” Kamanda Bonito alimaliza kumuangalia Peter kwa macho ya kumruhusu kuongea.



    “Familia yako ipo wapi?” Swali lilimtoka Peter na kumfanya Kamanda Bonito kutumbua macho kwa muda bila kulijibu bali kushikwa na butwaa.

    Naye Peter alijua kitu kama kile kitatokea, akamkazia macho usoni akionesha wazi anahitaji kujua familia ya mkuu yule ilipo.

    “Nikikwambia, utakuwa tayari kuwa mwanajeshi katika kambi yangu?” Kamanda Bonito alikuwa kausoma ubongo wa Peter vizuri sana kuwa kaja pale kutulia na si kuwa mwanajeshi na ndio maana badala ya kumuunga mkono Kamanda yule kwa mazoezi mapya ya kijeshi, yeye alirukia kwenye familia ya yule Mkuu.



    “Nitafikiria hilo.” Peter alijibu kwa kifupi.

    “Fanya maamuzi sasa.” Kamanda alikandamiza lengo Lake.

    Peter alishusha pumzi ndefu kabla ya kuchukua muda wa dakika kadhaa za kufikiria kama ajiunge au apotezee ombi la mkuu yule.

    “Okay. Nitakuwa mwanajeshi.” Peter aliafiki na kumfanya Kamanda Bonito atabasamu tabasamu pana usoni pake, kisha akaweka mikono yake mezani na kuanza kumsimulia historia ya maisha yake.

    *******



    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    HISTORIA YA KAMANDA BONITO MUCHAKILA.

    MIAKA ILIYOPITA.



    Kulikuwa na mvua kubwa usiku huo, mvua iliyokuwa imeambatana na upepo mkali pamoja na radi rasha-rasha zilizoangaza pande zote za anga ya Kameruni kama Malaika washukao toka mawinguni.

    Ni usiku ambao Kamanda Bonito hawezi kuusahau katika maisha yake kwani ndio usiku ambao familia yake iliteketea kama mshumaa uwakao sehemu yenye joto kali.

    Akiwa katikati ya usingizi mzito kwenye jumba kubwa la kifahari alilojenga Mzee Muchakila, baba wa Bonito ambaye alikuwa daktari bingwa wa nchi ya Kameruni, Bonito alisikia kelele za mwanamke zikitoka sebuleni.

    Aliposikiliza kwa makini, aligundua ni sauti ya mama yake. Sauti iliweza kupenya vizuri kwenye masikio ya Bonito licha ya mvua na ngurumo kali zilizokuwa zinaendelea kuchukua nafasi usiku ule.

    Bonito akiwa na umri wa miaka saba, alishuka toka kitandani alipokuwa kalala na kwenda kwenye mlango ambao ulikuwa haujafungwa kwa funguo wala komeo bali kurudishiwa tu.

    Bonito alitoka kwa tahadhari japo alikuwa mdogo, na kisha akaelekea mahali alipokuwa na uwezo wa kuona sebuleni kwao ni nini kinaendelea bila hata wale watendaji kushtukia kuwa wanaangaliwa.



    Katika ukuaji wake Bonito hakuwahi kusikia wazazi wake wakigombana, hivyo suala la mama yake kuendelea kutoa kilio kikali usiku ule, lilikuwa linampa mashaka na kujua wazi kabisa mama yake yupo katika mashaka na matatizo makubwa.

    Alifika sehemu ambayo alikuwa amepanga kushuhudia kinachoendelea pale sebuleni na kisha macho yake akayaelekeza huko.

    Hapo alishuhudia wanajeshi wapatao sita wakiwa wamesimama na mmoja wao akifunga zipu ya suruali huku mmoja akijiandaa kuishusha. Alipoangalia macho yao yalipoelekea, aligundua wanaangalia chini, na yeye akashusha macho yake wanapotazama wale wanajeshi ambao silaha zao aina ya bunduki za SMG zilikuwa pembeni.

    Pale chini alimshuhudia mwanajeshi mwingine akiwa juu ya mwili wa mtu huku kiuno chake kikipanda na kushuka kwa kasi. Maswali alijiuliza juu ya kinachoendelea pale chini na wakati huo alikuwa anashuhudia miguu na mikono pekee ya yule ambaye mwanajeshi yule alikuwa juu yake.



    Macho ya Bonito hayakuishia hapo, akayazungusha pembeni zaidi, hapo alimuona baba yake akiwa kakamatwa na wanajeshi wawili huku wakiwa wamekishika kichwa chake ili aendelee kuangalia ile picha ya yule mwanajeshi anayeshughulika kupandisha kiuno juu na kukishusha.

    Mzee Muchakila alikuwa analia kwa nguvu wakati hayo yanaendelea kutukia. Alionekana wazi kuwa anaumia.

    Macho ya Bonito hayakuishia hapo, akayazungusha tena kama mwenye kutafuta kitu. Na kweli alikipata, alikuwa anawatafuta dada zake. Mmoja akiwa ni wa tumbo moja na mwingine ni mfanyakazi wa ndani. Wote wawili walikuwa wamewekewa mtutu wa bunduki na mwanajeshi mwingine.

    Yule dada yake wa tumbo moja, alikuwa ni mwenye umri wa miaka miaka isiyozidi kumi na mitano. Naye alikuwa analia sana kila alipokuwa anamuona mama yake analia.

    Mara akamuona mwanajeshi yule wa viuno ananyanyuka pale alipokuwa anayarudi mauno. Macho ya Bonito yakalekea pale chini aliponyanyuka yule mwanajeshi. Hapo aliweza kuona nywele za kisogoni ambazo zilisukwa rasta, lakini hakuweza kuona sura mtu yule.

    Alijiuliza yule ni mama yake au labda mtu amekamatwa huko nje ndio wamemleta pale ili wamuoneshe baba yake jinsi walivyokuwa wakatili.



    Bonito akawa anaomba sala zake zote ili mtu yule ageuke. Na wakati anaomba sala hizo, alikuwa hataki sura ile iwe ya mama yake japo kwa asilimia zote ni lazima awe mama yake.

    Sala zake zilifika mahala pake kwani wakati mwanajeshi mwingine anapanda kifuani kwa mwanamke yule, mwanamke yule aligeukia upande aliokuwepo. Na hapo Bonito alikutanisha macho yake na mwanamke wa maisha yake, mwanamke aliyeteseka wakati anapata uzazi wake. Bonito alikutanisha uso na mama yake kipenzi.

    Mama yake alitikisa kichwa kwa shida pale chini alipokuwa kalazwa. Kichwa ambacho kilikuwa kinamkataza Bonito asiendelee kuangalia yale. Na wakati anafanya hayo, mara kafumba macho kwa nguvu na kutanua mdomo wake lakini hakutoa sauti kwa kuhofia mwanaye ataisikia na kuumia zaidi.

    Bonito akataka kujua sababu ya mama yake kuwa vile. Ndipo alishuhudia mwanajeshi mwingine akiwa kapanda juu ya kifua cha mama yake na kuanza kufanya kitu ambacho katoka kufanya mwanajeshi aliyepita.

    “Hii ni nini?” Bonito alijiuliza mwenyewe bila kupata jibu ya kile kinachoendelea pale sebuleni.

    “Mwacheni mke wangu jamani. Semeni manataka nini, nitawapa chochote.” Baba yake Bonito alitamka maneno hayo kwa sauti na kufuatiwa na kilio cha kwikwi.



    “Ooooh, unataka kujua tunataka nini?” Sauti nyingine iliongea na Bonito alikuwa hamuoni aliyeitamka kwani pale alipokuwa anachungulia hapakumpa nafasi ya kuona sebule zima japo ilikuwa ni sehemu njema ya kuweza kuona mengi ya sebuleni.

    Mara akamuona mtu anatokea pale mbele ya mwanajeshi yule aliyekuwa amemlalia mama yake. Kisha akampiga teke dogo yule mwanajeshi, naye mwanajeshi akasitisha zoezi la kupanda na kushuka kiuno chake kwenye mwili wa mama yake.

    Mwanajeshi akasimama na kurudisha kitendea kazi chake na kukifungia kwa zipu ndani ya suruali yake.

    Yule aliyeamuru mwanajeshi yule aache ile kitu, alikuwa kavaa tofauti na wenzake. Yeye alikuwa kavalia suti ya kijivu na shati la ndani lilikuwa ni jeusi pamoja na tai mwanana ya buluu huku kiatu chake cheusi king’aacho kama rami iliyooshwa kwa mafuta ya kupikia, kikimfanya aonekane maridadi kushinda wale wanajeshi.

    “Umesema utatupa chochote.” Aliongea yule maridadi.



    “Ndiyo nitawapa lakini mwacheni mke wangu.” Mzee Muchakila alijibu kwa hamasa na kuona kuwa kasikilizwa ombi lake.

    Maridadi yule alimuita yule mwanjeshi aliyekuwa kawawekea mtutu wa bunduki dada wa Bonito, na kisha alimuoneshea ishara ya kumwambia amlete yule dada wa tumbo moja na Bonito.

    Mwanajeshi yule akamkamata kwa nguvu yule mtoto wa kike na kumsukumia pale katikati ambapo mama yake alikuwa amelala huku macho yake yakiwa yamemuelekea Bonito pale kwenye kidirisha kidogo.

    “Unataka kufanya nini Mbucha, unataka kufanya nini Mbuchaaa?” Mzee Muchakila aliongea kwa sauti huku akijaribu kuinuka lakini alishindwa kufanya hivyo kwa kuwa alikuwa kakamatwa kwa nguvu na wale wanajeshi wawili.

    “Tafadhali usifanye hivyo Mbucha, nakuomba tafadhali.” Mzee Muchakila aliamua kuwa mpole kumsihi yule maridadi ambaye sasa alitambulika kama Mbucha.



    “Umesema utanipa chochote, na mimi nimetaka hichi.” Mbucha alimwambia Mzee Muchakila na hapo akampa ishara yule mwanajeshi aliyekatishwa raha zake kwa mama yake Bonito. Naye mwanajeshi akatabasamu tabasamu la kigaidi lakini lililoonesha furaha kwake.

    Akafungua suruali yake ya jeshi tena na kupiga mogoti mbele ya binti yule mdogo kwake. Binti ambaye kwa kulinganisha umri wao, yule mwanajeshi alimzidi miaka zaidi ya ishirini na tano.

    Yule gaidi akaanza kupapasa mapaja ya dada wa Bonito taratibu huku akisikia raha ya kupindukia na wakati huo Mbucha alikuwa anamuangalia baba wa Bonito ambaye alikuwa anakukuruka kwa nguvu kuonesha kuwa anapinga kitendo kile.

    Bonito akayarudisha macho yake kwa mama yake na hapo akakutanamacho yaleyale aliyozoea kuyaona tangu anakua. Macho ya kijasiri na maono ya mbali, lakini safari hii yalipoteza mwanga wa maono hayo.

    “Hapana Bon.” Bonito alisoma midomo ya mama yake ikimwambia hivyo.

    Mama yake alikuwa anamkataza Bonito asiendelee kuangalia matendo yale na badala yake aondoke pale alipokuwa.



    Bonito ni kama alikuwa haelewi ni nini mama yake anakifanya. Na hakuelewa chochote katika hilo. Hivyo alibaki pale alipokuwa amesimama na mara macho yake yalihama tena baada ya kuona kurupushani kati ya mwanajeshi na dada yake.

    Alipoangalia alimuona dada yake anakataa kufunuliwa sketi zaidi ya pale alipokuwa kafunuliwa. Mara alimuona yule mwanajeshi akizidi kutumia nguvu zaidi na alipoona yule mtoto wa kike anamzidi ujanja, ikabidi atumie mabavu yake.

    Alimuinua kichwa yule dada wa Bonito na kumtandika kofi zito ambalo lilimrudisha chini tena mtoto yule na hapo Bonito akapatwa na hofu kubwa. Akili yake sasa ikacheza na kuelewa kuwa familia yake ipo matatani.

    Macho akayaamisha haraka na kumwangalia mama yake.

    “Ondoka Bon.” Alisoma tena midomo ya mama yake ikimwambia aondoke pale. Lakini alishindwa kuondoka na macho yake yalivutika tena kuangalia pale dada yake alipolala. Safari hii alishuhudia yule mwanajeshi akimalizia kuitoa nguo ya ndani ya dada yake na mwanajeshi yule kushika kitendea kazi chake tayari kwa kukizamisha kwenye uzazi wa binti yule mdogo.

    “Kubakwa.” Akili ya Bonito iliwaza neno lile kwa kufananisha na tendo ambalo anafanyiwa dada yake.

    “Na mama pia kafanyiwa kitendo kile.” Bonito alizidi kuwaza na kuwazua bila kupata muafaka.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Naombeni jamani muiache familia yangu, tafadhalini jamani.” Mzee Muchakila alikuwa akiomboleza huku akilia kama mtoto mdogo lakini hakuna aliyemuelewa zaidi ya kushuhudia yule mwanajeshi akihangaika kuingia ukeni kwa yule mtoto mdogo aliyekuwa kapoteza nguvu kiasi baada ya kupigwa kofi kali.

    Yule mwanajeshi alifanikiwa kupata sehemu sahihi ya kuingiza kitendea kazi chake lakini alikuwa akipata upinzani mkubwa kutokana na ukuta mzito uliokuwa umekaza kwenye kizazi cha mtoto yule.

    “Tumia nguvu.” Mbucha alimwambia mwanajeshi yule kwa sauti naye ni kama alikuwa ndio kaambiwa ua. Akakaza kiuno chake na kwa nguvu nyingi ambazo anazo akaingia mwilini wa binti yule na kuanza kujijaza juu, chini kama anafanya na mtu mzima.



    Binti yule alipiga ukelele mmoja mrefu na ulipokwama, hakusikika wala kuonekana akicheza zaidi ya yule mwanajeshi kuzidi kujichimbia ndani ya uzazi wa yule binti hadi akamaliza shida zake.

    Mwanajeshi alisimama huku akitabasamu kwa furaha na kufunga zipu yake.

    Akaanza kumpiga mateke madogo binti yule kuona kama ataamka lakini hakuamka zaidi ya kuendelea kumwaga damu pale chini zilizotoka katika kizazi chake.

    “Good, soldier. (Vizuri, Mwanajeshi).” Ndivyo Mbucha alimwambia yule mwanajeshi huku anampigapiga begani baada ya kuona hali ya yule binti.

    Yule mwanajeshi akatabasamu kwa tabasamu la ushindi hasa alipoona kasifiwa na mkuu wake. Akarudi nyuma na kusimama sawia na wale wenzake ambao walikuwa wanampongeza kwa kumpa tano.

    Bonito akazidi kuangalia ile filamu ambayo kwa sasa alianza kuielewa japo mama yake alizidi kumkanya aondoke pale. Baba yake alikuwa analia kwa nguvu huku akiwa kakamatwa mikono yake na kushikwa kichwa ili asiangalie kwingine zaidi ya yale maovu ya pale.



    “Unajidai Daktari bingwa wa nchi, sasa leo tunataka kukuona utaweza kuwatibu hawa wenzako na kujitibu wewe mwenyewe?” Mbucha aliongea na kumfanya Bonito atoe macho yake kwa mama yake na kumwangalia mtu yule ambaye kwa makadirio alikuwa na miaka isiyozidi thelathini na tatu.

    “Muue huyu.” Mbucha alimuru yule mfanyakazi auawe na kabla hata yule mfanyakazi hajatamka lolote, alishtukia risasi ikipenyeza kichwani kwake.

    Hapo Bonito alishtuka kama aliyetoka ndotoni hasa kwa ile risasi ambayo sidhani kama majirani waliisikia kutokana na mvua kubwa iliyokuwa inaendelea nje pamoja na umbali wa nyumba zao. Ila kwa mle ndani ilisikika kwa kuwa vigae vilivyoezekwa juu ya nyumba ile, vilipunguza sauti ya mvua ile kubwa.



    Bonito bila kujijua, alijikuta anaanza kutengeneza hisia za hasira juu ya mtu yule. Hasira hizo ziliamia hadi kwenye chuki ambayo baadae alikuja kugundua anahamu ya kulipa kisasi kwa yale anayoyashuhudia utotoni.

    “Ondoka Bonito.” Mdomo wa mama yake ulizidi kusisitiza hilo baada ya Bonito kumwangalia tena wakati huo yule mwanajeshi aliyemuua mfanyakazi wa ndani, alihama ile sehemu ambayo alikuwa kawashikilia wale wasichana wawili.

    “Muue na huyo.” Mbucha alimuru mama wa Bonito auawe naye wakati yule mwanajeshi anapita mbele yake.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog