Search This Blog

Sunday 22 May 2022

KITANZI CHA MWISHO - 4

 







    Simulizi : Kitanzi Cha Mwisho

    Sehemu Ya Nne (4)



    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kwa kutumia ngazi za nje, Kamanda Amata alimshika mkono Yaumi na kuteremka nae kwa haraka. Alipofika mwishoni tu, ilikuwa ni kitendo bila kuchelewa, Land Cruiser Prado ilikuwa imesimama mbele yake, vyoo vyeusi, kwenye usukani kulikuwa na mwanamama mtu mzima, mlango ukafunguliwa, Yaumi akapakiwa ndani kisha Kamanda Amata akafuatia, Madam S akaitoa gari ile kwa kasi. Alizipita nyumba za maafisa wa magereza na kukunja kushoto akiuacha uwanja mkubwa wa mpira na kuteremkia katika bustani za michicha alipofika karibu na bwawa la maji machafu akapunguza mwendo, mlango wa pembeni kushoto ukafunguliwa, Chiba akajitoma ndani na gari ile ikaendelea kuchanja mbuga mpaka eneo la Kipunguni. Akachukua barabara ipitayo pembezoni mwa ofisi za mamlaka ya hali ya hewa, akatiririka nayo mpaka barabara kubwa ya Pugu na kupinda kulia kuelekea mjini. Wakiwa Tazara katika foleni ya kuelekea mjini, pembani yao ikasimama gari nyingine aina ya Land Rover 110, “Nifuateni,” ilikuwa sauti ya Madam S iliyokuwa ikiamuru, wakatia huo alikuwa tayari amekwishashuka na kuiacha gari hiyo ikiunguruma kwenye foleni. Kamanda Amata akashuka huku mkononi mwake kamkamata Yaumi na kuingia kwenye ile Land Rover pamoja na Chiba, Yule dereva wa ile Land Rover akaingia kwenye Prado, safari ikaendelea.

    “Yaumi usiogope, upo kwa watu salama kabisa,” Amata alimwambia Yaumi huku akimvisha guo jeusi usoni, safari yao ikaishia ‘shamba’ huko Gezaulole katika ofisi yao nyeti iyatumika pia kuhifadhi watu kama Yaumi ili wasionekane na jamii

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    <<<<< ndugu msomaji, nimekuwekea kipande hicho hapo juu ili upate muungano wa riwaya hii, kutoka kipande cha 23 na kipande cha 1.

    Sasa endelea episode ya 24, Stori ndo kwanza inaanza...>>>>>



    EPISODE 24



    MADAM S alimtazama Yaumi kwa kumkazia macho, kisha akamgeukia Kamanda Amata aliyekuwa ameketi mkabala na mwanamke huyo. Simulizi hiyo aliyoitoa kwa wanausalama hao ilitikisa moyo wa kila mmoja. Yaumi aliwatazama Madam S na Kamanda Amata kwa zamu, akashusha pumzi na kuegemea kiti alichokuwa ameketi.

    “Ukapumzike Yaumi, umechoka sana, daktari wetu atakuja kukupa matibabu muda si mrefu,” Madam S alimwambia Yaumi huku akimpa ishara ya kumfuata, Yaumi akainuka kwa msaada wa Kamanda Amata, akatembea taratibu na kumfuata Madam S, huko akaoneshwa chumba chenye kila kitu, maji safi ya kuoga, nguo za kubadilisha na kila kitu. “Hapa ndipo patakuwa kwako kwa muda, upumzike vya kutosha kisha baadae utaongea na Kamanda Amata ili kujua wapi pa kuanzia katika kutatua swala lako, usiogope kuwa huru, omba na uliza unachotaka, ila simu hautoruhusiwa kupiga nje ya jengo hili,” Madam S alimwambia Yaumi kisha akamuacha na kuondoka.

    Kwa Yaumi ilikuwa ni kama muujiza, hakuamini kila kinachotokea katika maisha yake, alikitazama kile chumba kilikuwa na kila kitu ndani, bafu la kisasa, nguo za kubadilisha, jokofu lililojaa vinywaji vya aina aina.



    Kamanda Amata alitulia kimya akitafakari hali hiyo, Madam S aliketi mbele yake, akamtazama kijana huyu aliyeonekana wazi kuchoka kwa mambo mengi. Chiba nae aliungana nao hapo mezani, jopo hilo la watu watatu.

    “Sina budi kuwapongeza kwa kazi ngumu mliyoifanya leo, hakika kwa anayejua kilichofanyika leo basi hana budi kukiri kuwa Tanzania tuko juu katika idara ya kijasusi, kama ingekuwa ni lile taifa babe la ulimwengu, lazima lingeleta makomandoo wasiopungua saba kwa kazi ambayo ni ndogo sana, lakini vijana wangu wawili mmefanya kazi nzito kwa dakika mbili tu na kuikamilisha, haijawahi kutokea na mnastahili pongezi,” Madam S aliwapongeza vijana hao wakakamavu kwa kazi hiyo ya kumuokoa Yaumi, Sasa Kamanda Amata utaongea taratibu na Yaumi ili ujue ni wapi pa kuanzia sakata hili, ili kila atakayehusishwa achukuliwe hatua.

    “Madam S, hapa kwanza ni kumalizana na Yule mhudumu wa bar kule ili kutoka kwake ijulikane ni nani anafanya haya chinichini, kisha tutapanda taratibu ili kujua ukweli” Kamanda Amata alijibu.

    “Lakini Kamanda una uhakika kifo cha ACP Chonde kina uhusiano na kesi ya Yaumi?” madam akauliza tena.

    “Ndiyo, nina uhakika kwa sababu kwa nini auawe wakati anashughulikia kesi hiyo na si wakati mwingine,?” Amata akajibu kwa swali.

    “Na kwa vyovyote katika jeshi hilohilo la polisi inawezekana kabisa kuwa kuna mtu anayetoa siri ya muenendo wa kesi kwa adui wa Yaumi ndiyo maana wanajua ni nani anafanya nini katika hili,” Chiba aliongeza maoni yake.

    “Nimewaelewa makamanda wangu,” Madam S alijibu, akakohoa kidogo kusafisha koo kisha akaendelea, “Sasa nani anaanzia wapi na wapi anaanzia nani?” akauliza.



    Wote wawili yaani Chiba na Amata wakajipanga sawia jinsi ya kuanza kufuatilia kesi hiyo A mpaka Z na kuhakikisha wanajua mbivu na mbichi, “Kitengo mnachofanyia kazi hakimuogopi mtu, awe waziri awe mbunge awe Rais, kama anahatarisha usalama wan chi lazima ashughulikiwe ndicho kiapo mlichoapa, sivyo?” Madam S akawauli akiwa amesimama akiwatazama kwa macho yake makali, “Ndivyo, Madam,” wakajibu kwa pamoja.

    Walimuacha yaumi akiendelea kupumzika, na wao wakaondoka zao kutoka katika jumba lile, Madam S alibaki kwa kazi nyingine katika ofisi hiyo ya siri.

    Saa moja tu ilimfikisha Kamanda Amata katika kituo cha polisi cha Tabata, alipofika pale na kumuulizia Yule kijana CID akaambiwa kuwa ametoka kwa majukumu ya kikazi, hivyo arudi baadae, akatii na kurudi katika gari yake. Safari ya kuelekea katika gereza la Segerea ikaanza, akiwa na mawazo mengi kichwani lakini bado akitafakari kazi ya hatari walioifanya siku ile katika gereza la Ukonga, Kamanda Amata aliona wazi kuwa mbele anakabiliana na kazi nzito kama sio kubwa. Akapita eneo la kituo cha daladala cha Segerea na kupandisha kilima kidogo kisha akakunja kulia na kuingia katika uwanja wa magereza, akaegesha gari panapotakiwa na kuteremka, japokuwa alikuta askari waliokuwa katika vikundi vikundi lakini hali hiyo haikumsumbua kichwa alijua tu ni nini wanachojadili, alivuta hatua ndefundefu na kuilekea zahanati ilikua ikimtazama mbele yake, hakuwa na haja ya kuuliza kwani maandishi makubwa yaliyosomeka ‘ZAHANATI YA MAGEREZA’ yalimuongoza kuwa hapo ndipo.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Habari yako afande,” alimsalimia askari mmoja wa kike aliyekuwa ameketi katika kiti kilichotanguliwa na meza ndhifu ya Formica

    “Nzuri, karibu nikusaidie nini?” aliitikia na kumuuliza Kamanda.

    “Naweza kumuona Dr Omongwe?” akauliza.

    “Ndiyo, bila shaka, nimwambie nani?”

    “Mwambie, ACP Jaffary kutoka kituo cha polisi kati,” Kamanda akajibu. Yule mwanadada akamtazama kwa chati kijana huyu mwenye kifua kipana cha mazoezi kilichomfanya aonekane kuwa na siha nzuri inayovutia mrembo yoyote duniani.



    Akanyanyuka kutoka kwenye kiti chake na kuingia mlango namba 3, dakika mbili tu akatoka na kumpa ishara ya kuingia, Kamanda Amata akajitoma ndani na kukutana na daktari huyo aliyekuwa akitaka kuonana nae, hakujua ni nini anataka kumwambia lakini kichwa chake tayari kilianza kupanga maswali na majibu. Akavuta kiti na kuketi akitazamana na Dr Omongwe aliyekuwa ndani ya mavazi ya magereza, shati jeupe lenye vifungo vya chuma na sketi ya rangi ya udongo iliyokolea, juu ya yote hayo alivalia koti jeupe kuonesha kuwa yeye ni mdau wa afya, kofia aina ya barret ilitulia kichwani mwake ikiwa katika mtindo nadhifu, ikiwa imeinamia kidogo upande mmoja na kuruhusu nywele zake zilizosukwa kwa mtindo wa kimasai kuning’inia na kudhihirishurembo wa mwanadada huyu.

    “Karibu sana, naitwa Dr Omongwe,” alijitambulisha

    “Asante sana, naitwa ACP Jaffary, kutoka kituo cha polisi kati,” kamanda Amata akajitambulisha kwa jina lake na cheo bandia kama ilivyo ada kwa watu wa kazi kama yake.



    “Karibu afande nakusikiliza,” Omongwe alijiweka vizuri. Kamanda Amata akachomoa peni yake kutoka katika mfuko wa shati, akachukua kipande cha karatasi na kuiminya sehemu ya juu ile peni kama mtu anayetaka kuandika, kumbe hapana kwa kuiminya vile ni kuruhusu peni ile iweze kurekodi kila linalozungumzwa, peni ya kijasusi, yenye uwezo wa kurekodi sauti mpaka ukubwa wa GB 8 lakini pia unaweza kuitumia kwa kuandika.

    “Utanisamehe afande, nina maswali kidogo napenda kujua, kama ambavyo unajua kuwa kijana wetu ACP Chonde ameuawa,” kabla Kamanda Amata hajamaliza kujibu, Dr Omongwe alimkatisha, “Sasa afande, katika hilo mimi ninahusika vipi? Mbona simjui huyo aliyeuawa,” akauliza na kutulia.

    “Dr Omongwe, unanitia mashaka, kwa kuwa wewe ni mwana usalama lakini inaonekana haupo radhi kunipa ushirikianoa, kama humjui mtu huyo aliyeuawa, kwa nini uliokwenda makaburini kuzika?” swali hilo la Kamanda Amata lilionesha wazi kumpa mshtuko Dr Omongwe, akatulia na kuvuta hisia zake kuzikusanya na kuweka sawa, Kamanda akaendelea kumwambia, “Mimi kuja hapa si kwamba nimekosea, bali ninajua ninachotaka kufanya, nimekuona na hivi ninavyokwambia nimetoka kumhoji WP Magreth wa polisi Kimanga ambaye jana kuna kipindi mlikuwa pamoja pale makaburini mkiteta jambo, tunataka kutatua tatizo, lakini kwa nini unataka kutumia uongo ili kukwamisha?” Kamanda alihoji sasa kwa ukali ijapokuwa alimdanganya kidogo.



    “Uhhhhhh!!!!!” Dr Omongwe alishusha pumzi huku akiitoa kofia yake na kuiweka mezani kisha akajiweka vizuri na kumkabili Amata, “Haya sema hasa hasa shida yako ni nini?” akauliza.

    “Ninapenda kujua uhusiano kati yako wewe na marehemu, hilo tu basi, sisi tunamtafuta muuaji na najua wewe humjui lakini majibu yako yatatupa mwanga,” Kamanda alianzia alipoishia.

    “Mimi sina uhusiano na marehemu, isipokuwa siku mbili kabla ya mwili wake kuokotwa, marehemu alikuja hapa ofisini kunihoji kama wewe ulivyofanya, alipotoka hapa basi, baadae nikasikia kuwa ameokotwa amekufa ndiyo maana nikaja kuzika,” Dr Omongwe akajibu.

    “Sawa, naomba uniambie alikuja kukuhoji juu ya nini? Naomba unijibu kwa kuwa ukinificha kuna mlolongo wa wtu watakaokufa, lakini ukinijibu ukweli utakuwa umeokoa roho nyingi sana,” Kamanda alitumia lugha ya kushawishi, akamtazama Omongwe aliyeonekana kuwa na matone machache ya jasho katika pua yake.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Alikuja kunihoji juu ya mwanadada mmoja naliyekuwa hapa mahabusu lakini yuko nje kwa dhamana, anaitwa Yaumi,” Omongwe akajibu.



    “Yaumi? Yaumi yupi?” Kamanda akauliza wakati akijua kabisa anamzungumzia Yaumi yupi.

    “Kuna Yaumi alikuwa hapa mahabusu, alikuwa na kesi ya mauaji ya mumewe, ijapokuwa alikuwa nje kwa dhamana lakini inasemekana kuwa aliendelea na mauaji kwa watu wengine, sasa marehemu Chonde alikuja hapa magereza kutafuta ukweli kama huyo mwanamke akiwa chini ya ulinzi wa askari magereza je alikuwa anaweza kutoka nje kwenda uraiani na kufanya mauaji? Ndi cho hasa alichokuwa akihoji, akafika kwangu kwa kuwa siku inayosemekana kuwa kuna mtu aliuawa nyumbani mwake huko Kimanga, yeye alikuwa mahabusu lakini siku hiyo alikuwa anaumwa sana hivyo alilazwa hapa na mimi mwenyewe ndiye niliyemhudumia usiku wote,” Dr Omongwe alijibu kwa kirefu jibu ambalo lilimpa mwanga Kamanda Amata.

    “Sikiliza Omongwe, waliomuua Chonde wanakutafuta na wewe, hivi jana ilitakiwa uuawe, unalijua hilo?” Kamanda Amata akamuuliza kisha akamtazama atalipokeaje. Dr Omongwe alitulia kimya, mawazo ya ghafula yakakigubika kichwa chake, ubaridi ukapenye kuanzia nutosini mpaka unyayoni, akamtazama Amata.

    “Rudia unachosema,” Dr Omongwe akaomba huku akionekana wazi kuishiwa nguvu. Kamanda Amata akamtolea kivuli cha barua ile aliyopewa Chilungu muuaji, akampatia Omongwe naye akaisoma mara nne nne kupata uhakika.



    “Mpaka sasa upo hai kwa kuwa jeshi la polisi linathamini uhai na kazi yako, limemkata muuaji na limemuweka ndani, sasa nilitaka kujua kama kunauhusiano zaidi na marehemu Chonde ili tuunganishe kwa nini wanataka kukuua na wewe, umenielewa sasa?” Kamanda alipouliza swali hilo, Omongwe alitikisa kichwa kuahiri ameelewa, lakini macho yake yalikuwa yamejawa machozi ambayo yalisubiri nukta chache tu yamwagike.

    “Kwa hiyo?” akauliza.

    “Kwa hiyo lile ulilomwambia Chonde basi ndilo lililomuua, na hilohilo kwa kuwa wewe unalo ndio maana wanakutafuta, tumemkamata muuaji lakini sina uhakika kama yuko peke yake, uwe na hadhari kubwa, usitembee ovyo peke yako, wala nyumbani usikae peke yako,” akiwa katika kusema hayo mara mlango ulifunguliwa bila hodi, afande Marina akaingia, “Vipi afande? Mbona hivyo bila hodi jamani?” Dr Omongwe akamuuliza, “Ah samahani, sikujua kama kuna mtu,” akajibu na kuufunga mlango nyuma yake.

    “Huyu ni nani?” Amata alihoji.

    “Ni afande tu ila ana tabia za umbea sana, hata siku nilikuwa na Chonde hapahapa aliingia hivyohivyo, hana lolote basi tu,” Omongwe akajibu. Akili ya Kamanda ikafanya kazi haraka, ‘Anaweza kuwa pumba kama sio mahindi’ akajiwazia mwenyewe, “Anaitwa nani?” akauliza.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Anaitwa Marina,” Omongwe akajibu.

    “Asante sana, basi mimi naomba niende nitakapokuhitaji basi nitakupigia simu, naomba tusaidiane sana katika hili,” kamanda Amata alimuomba Omongwe kisha wakabadilishana namba za simu, wakati Kamanda alipokuwa akitoka, Dr Omongwe alimuita naye akageuka, “Chonde alitoka, sikumuona tena, na wewe uwe makini tafadhali, taifa linakuhitaji,” yalikuwa maneno ya Dr Omongwe kwa Kamanda, tabasamu pana liliashiria kupokelewa ujumbe huo katika moyo wa mpelelezi huyu, akatoka na kuufunga mlango kabla ya kumuaga Yule mwanadada wa mapokezi, “Asante sana mrembo, mi nakwenda,” akavuta hatua kuondoka lakini kabla hajashuka ngazi, akasimama ghafla na kugeuka nyuma, akarudi mapokezi na kuingiza mkono mfukoni akatoa waleti yake iliyotuna kwa noti za Kitazania akatoa noti ya elfu kumi akaambatanisha na kadi yake ya kibiashara, akampatia Yule dada wa mapokezi, kwa sauti ya chinichini akamwambia, “Nitafute baadae mrembo,” kisha yeye akaendelea kondoka. Yule mwanadada, afande wa mapokezi aliipokea ile kadi na pamoja na ile pesa, labda ingekuwa kadi peke yake angeikataa lakini na elfu kumi juu, ukizingatia ni tarehe dume, akazisunda mfukoni bila kuangalia vizuri…



    BAADA ya kizaazaa kilichotokea katika chumba cha kitanzi, wakuu wale wa vikosi vya ulinzi na usalama walikutana falagha kutathmini tukio hilo. Mchana huo kila mtu alikuwa hana majibu, chumba cha mkutano kilikuwa hakitoshi, maana kilionekana ni kidogo mno kwa jinsi hoja hiyo ilivyokijaza. Kamisna wa Magereza alikuwa ndiye muongeaji mkuu katika mkutano huo.

    “Kwa kweli ni kitendo ambacho hakijawahi kutokea katika historia ya nchi hii, hata hapa nikifikiria, bado sipati jibu kabisa, ni nini kimetokea! Chini ya ulinzi mkali wa magereza, hawa watu wamepitia wapi kuingia? Hii ni hujuma au njama,” Kamishna aliongea kwa ukali akionekana wazi kugadhibika kwa hali hiyo.

    Gabriel Matinya alikaa kwa utulivu kabisa, alionekana wazi kushangazwa kwa na hali hiyo, mara nyingi matukio kama haya ambayo yametokea kwa Yaumi, yeye alihusika kwa kutumia vijana wake, lakini lililotokea leo mbele ya macho yake alikiri moyoni kuwa kuna watu wamejipanga kwa kazi za hatari, alijuwa wazi kuwa watu waliofanya hilo hana uhusiano nao, swali likabaki kichwani mwake, ni nani na kwa nini tukio hilo limetokea. Mkuu wa majeshi alikuwa ameshika tama akitafakari hali hiyo, alikurupuka pale aliposikia njina lake likitajwa, “Da kwa kweli nikiangalia tukio hilo nakumbuka sinema inayoitwa Fifty Fifty, nafikiria kama nilikuwa naangali hiyo sinema au nimeona tukio la kweli, ule ni ugaidi, tena ugaidi wa kimataifa, sasa nani kaendesha operesheni hiyo, kwa nini, hatujui, tumekwisha, kama mfungwa anachukuliwa mbele yetu, katika mikono ya askari wa majeshi yote kiulaini namna ile, basi twendeni tukailinde Ikulu kwa batalioni tatu za jeshi,” aliongea na kisha kutikisa kichwa kwa masikitiko.



    Baada ya majadiliano ya muda mrefu, askari wote waliokuwa zamu siku ile waliitwa na kufanyiwa mahojiano ya ana kwa ana, mmoja baada ya mwingine. Hakuna aliyeonesha kujua lolote katika hilo, baada ya kuwahoji kwa kina ikabidi sasa wachague jopo la askari wakateua na wachache kutoka jeshi la polisi ili kufanya uchunguzi katika mipenyo yote ya gereza taarifa itolewe kwa jopo hilo ndani ya siku tatu, utata.

    “Aibu sana, inabidi vyombo vya habari visiandike habari hii, ni aibu,” alisema kamishna wakati akiingia katika gari yake tayari kwa safari ya kurudi ofisini, makao makuu ya Magereza. Gabriel Matinya alionekana wazi kuchanganyikiwa kwa uzito mkubwa kwa swala hilo, alikuwa akijiuliza nani aliyefanya tukio hilo, ina maana kuna watu wengine waliokuwa wakimuinda Yaumi? Swali gumu. Aliondoka katika eneo la gereza akifuatiwa na mkuu wa mkoa na Yule wa wilaya, wao moja kwa moja waliekea Ikulu kutoa taarifa hiyo kwa mkuu wa nchi.



    “Siamini mnachoniambia, mbona ni kama riwaya za Richard Mwambe kwa jinsi lilivyo?” Mkuu wan chi alimuuliza mkuu wamkoa ambaye alikuapo kwenye tukio lile. “Hii nchi siku hizi kila kitu kinaweza kutokea, nimwamini nani katika ulinzi wan chi?” alijisemea huku akiwa ameinamia mezani. Mkuu wa mkoa alimpa wazo la kuitisha wakuu wa vyombo vya usalama nchini ili kupata suluhisho na jinsi ya kuanza uchunguzi ili kujua ni nani amehusika au kikundi gani kimehusika, kama Al-Qaeda, Boko Haram, Al-Shabab, Anti Baraka au ni kikundi gani na kwa nini.

    “Haina haja mheshimiwa, achana na hilo halitasaidia, hata nikiwaita nitawaambia tu waimarishe ulinzi hapa Ikulu na kwenye idara nyeti, najua ni nani wa kumuita na anayeweza kutekeleza kazi hii kwa ufanisi,” Mkuu wan chi aliongea kwa unyonge kisha wakaagana na mkuu wa mkoa akimuahidi kuonana naye siku inayofuata. Mkuu wan chi akajiinamia mezani, hofu kuu ya usalama wa nchi anayoiongoza. Alitafakari kwa kina lakini jibu lilikuwa kitendawili, amiri jeshi mkuu alibaki akifikiria nini cha kufanya.



    §§§§§

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Nimekuiteni hapa kwa jambo moja nyeti sana, ijapokuwa watu hawajui kilichotokea na kwtu tumekifanya siri, lakini sina budi kuwaambi ninyi askari wangu wa miamvuli ili muingie kazini mara moja, Yaumi hajanyongwa,” Matinya alikuwa akiwaambia vijana wake, akawatazama kwa jinsi walivyopigwa na butwaa, “Ametekwa katika hali ambayo mpaka sasa sisi wenyewe hatujui ni nani aliyefanya hilo, naomba muingie kazini mumtafute awe ndani au nje ya nchi,” Matinya akashusha pumzi na kuusikiliza ukimya uliotawala katika chumba hicho, akaendelea, “Mpango wetu ulikuwa pia Dr Omongwe afe kabla ya leo, lakini nasikitika kuwaambia kuwa bado yupo hai, inaonekana kuna tatizo hapa, nalo lifanyiwe kazi mara moja, ikiwezekana auawe,” Matinya bado alikuwa akiongea kwa taabu kidogo huku akionekana kuloa jasho mwilini, presha ilikuwa inapanda na kushuka bila mpangilio maalumu.

    “Boss!” Scogon alimwita Matinya, wakatazamana, “Uwezo wetu ni mdogo sana kuweza kumtafuta Yaumi kama atakuwa ametekwa na watu wenye taaluma hiyo kwa kiwango cha juu, tunaweza tukatumia muda mwingi sana na mambo yakaharibika, we unalionaje hilo?” akauliza.



    “Nimekuelewa, nafikiri itabidi tukodi mtaalamu atakayeweza kutusaidia katika kazi hili, sasa sijui tuangalie wapi, Israel, Urusi, Ureno, Somalia au wapi sijui, lakini liache nitakupa jibu usiku nikikutana na mtu wangu muhimu kwa kazi hiyo,” Matinya akamaliza na kuagana na vijana wake akiomba asisumbuliwe kwa muda kwani anahitaji kupumzika.

    Scogon aliwatazama vijana wake, kikosi kazi, wote aliwaona wapo katika hari ya kazi na si vinginevyo, “Tunaingia kazini, hakikisheni mnamtafuta Yaumi kwa siri chinichini na kila jibu mnipe mara moja,” baada ya kupewa kazi hiyo wakatawanyika.

    Scogon alimalizia kinywaji kilichojaa katika glass yake, akaitua glass na kuiacha mezani wakati yeye akitoka nje ya nyumba hiyo, katika ngazi za kupandishia barazani akakutana na Marina ambaye ndiyo kwanza alikuwa amefika katika nyumba hiyo, “Vipi? Mzee yupo?” Marina akamuuliza Scogon, “Yupo ila kasema asisumbuliwe,” akajibiwa. Ijapokuwa aliambiwa hivyo lakini alipitiliza mpaka katika chumba ambacho Matinya hupenda kupumzika, akasukuma mlango na kuingia ndani kisha akaufunga kwa ufunguo nyuma yake.

    “Marina, afadhali umekuja dear wangu, leo njiko vibaya sana hata sijielewi nafanya nini na naacha nini” matinya alimwambia yaumi huku akimshika mkono kumvutia kitandani, akambusu, “Nipe yaliyojiri magereza,” akamwambia.

    “Aaaah mpenzi, my sweetheart, mbona Omongwe hajafa ni mzima mpaka sasa, halafu leo alikuja kutembelewa na ACP Jaffary kutoka kituo cha polisi cha kati, niliwakuta wakiongea maswala haya haya hasa kifo cha Chonde,” ilikuwa ni habari nyingine iliyoleta mshtuko kwa Matinya, “ACP Jaffary,” akarudia jina hilo huku akitafakari. “Nahisi mpango huu umeshakuwa mgumu,” aliongea tena kwa upole huku akiwa kamuegemeza Marina kifuani pake. “Mpango gani mpenzi, mbona siku zote hutaki nkunambia?” Marina aliuliza, lakini Matinya alichukua muda kujibu.

    “Marina, una hati ya kusafiria?” Matinya alimuuliza Marina, “Hapana sina kwani vipi?” naye aliuliza.

    “Kila siku nakwambia hutaki kunielewa, nitakuacha hapa wakati mi nahamia nchi nyingine siku si nyingi,” Matinya akaeleza, “Na kwa nini uhame?” akauliza.

    “Shauri yake, mwenye macho haambiwi tazama,” Matinya alimalizia maneno yake na kujizungusha upande mwingine kisha akafumba macho kuutafuta usingizi.



    §§§§§



    “Naomba nitajie majina ya wote unaoona wanaweza kuwa watuhumiwa katika kadhia hii ili nianze mmoja baada ya mwingine,” Kamanda Amata alimwambia Yaumi wakati wakiwa wameketi sebuleni katika ofisi nyeti huko ‘Shamba’.

    “Kamanda kwanza kuna mdada anaitwa Marina ni askari wa jeshi la Magereza pale Segerea, huyu kwa vyovyote anajua kitu, maana alikuwa akinifuatilia sana gerezani na kunipa maneno ya kejeli, kuniita mi muuaji,” Yaumi alikuwa akiongea huku akisikitika sana. “Ok, Marina, na mwingine ambaye una wasiwasi naye…” Kamanda aliandika pembeni na kuendelea kuuliza.

    “Kwa kweli ukiacha Yaumi, nitakuwa muongo kujua majina ya wengine, kati ya ninowahisi ni mmoja namkumbuka sana kwa sura, huyu ndiye nilimuamuru kuteremka pale Morocco,” Yaumi akajibu.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ok, baadae mtaalamu wetu atachora picha ya huyo mtu kwa maelekezo yako ili tuitambue, haya niambie unamfahamu anaitwa Omongwe? Daktari wa jeshi la Magereza” Kamanda akauliza.

    “Ndiyo, ni rafiki yangu sana, nilikuwa nae JKT, yeye alipoingia Magereza mimi nikapata mchumba na kuolewa, na alikuwa ananisaidia sana mimi kutoka nje” Yaumi akajibu. Kamanda Amata akaandika tena kwenye kijitabu chake cha kumbukumbu, akaichomoa peni yake na kuunganisha kidubwasha cha kuvaa sikioni akampa Yaumi asikilize mazungumzo yake na Omongwe. Baada ya kumaliza kusikiliza, alimuona Yaumi kama mtu aliyepigwa na shoti ya umeme, “Walitaka kumuua?” akauliza, “Kama ulivyosikia,” kamanda akajibu. “Tafadhali msaidie,” Yaumi alilalama, “Usijali, yuko katika ulinzi hawawezi kumuua,” Amata akampa moyo.

    “Yaumi naomba uniambie, Uganda ulikwenda kufanya nini?” Kamanda aliendelea kuhoji kiurafiki zaidi hali mbayo ilimfanya Yaumi kujibu bila woga.



    “Mume wangu kabla hajafa kuna namba aliniandikia, lakini kabla hajanifafanulia juu ya namba hizo akakata roho, kwa maana alinambi akuwa kuna jambo zito anataka kunieleza, lakini hakufanikiwa, mimi sikuwa najua juu ya namba hizo, nilizinakili pembeni, nikiwa mahabusu nikapata rafiki mmoja kiziwi anaitwa Fasendy, yeye aliachiwa baada ya kukosekana ushahidi huyu mwanadada alikuwa akija kuniletea chakula mara kadhaa, akanielekeza nyumbani kwake, siku nilipotoka kwa dhamana alinikaribisha kwake nikalala pale siku kama mbili hivi ndipo aliponambia kuwa zile namba kwa jinsi zilivyopangwa ni namba za posta pale Kampala, kwa sababu alisema namba tatu za kwanza ni zinamaanisha Uganda zilikuwa ni + 256 na iliyofuatia ilikuwa na tarakimu tano 16841 baada ya kuitafakari kwa muda huyu dada akanambia itakuwa ni namba ya sanduku la posta, na ile ya mwisho ilikuwa ni tarakimu nne 5576 akanielekeza kuwa hizo ni namba za mtaa na majengo, hivyo akaniambia mpaka ofisi gani ya posta yenye hilo sanduku kutokana na na mpangilio wa hizo namba,” Yaumi alieleza kwa ufasaha kabisa. Kamanda Amata akabaki kinywa wazi akijiuliza jinsi huyo mwanamke anavyoweza kuzichambua hizo namba kwa ufasaha kujua mpaka zinamaanisha nini na kiko wapi, akaona wazi kuwa huyo si mwanamke wa kawaida, hata yeye pamoja na kazi yake ya kikachero bado asingeweza kwa wepesi huo kujua maana ya namba hizo. “Yaumi umesema huyu dada anaitwa nani?”

    “Anaitwa Fasendy, anaishi Bunguruni kwa Mnyamani nyumba namba BGN/MNI 612 B,” Yaumia akajibu.

    “Ok, na pale posta Kampala ulichukua nini?” Swali linguine.

    “Hakukuwa na kitu kabisa ndani ya lile sanduku,” akajibu.

    “Baada ya kuona hakuna kitu ukaweka bomu, ulilipata wapi?” Kamanda akauliza huku akicheka.

    “Hamna, mi nilipoona lile jamaa linang’ang’ania nikaliacha na kukimbia, ni usiku wake mi naambiwa kuwa nimeweka bomu,”

    “Ok, nimeshajua, asante kwa majibu haya ya awamu ya kwanza, nahitaji kuonana na Fasendy mapema ya kesho ili nae anipe machache,” Kamanda Amata alisema hayo akiwa amenyenyuka tayari kwa kuondoka, ilikuwa ni saa mbili ya usiku….





    MADAM S alimwita Kamanda Amata nyumbani kwake Masaki usiku huo kabla ya yote. Wakati Kamanda Amata akiingia katika lango kuu la nyumba hiyo ilikuwa ni muda mfupi tu tangu Madam S aingie. Kama kawaida yake, alifungua mlango wa mbele kwa namna anayojua yeye na kuingia katika sebule kubwa yenye kila kinachohitajika kuwamo. Moja kwa moja akaliendea jokofu lililopo hapo sebuleni na kutoa kinywa ji murua cha Safari Lager na kuketi kwenye sofa kubwa. Sekunde chache Madam S aliungana nae. “Kamanda! Nilikuwa nimeitwa Ikulu,” Madam S akaanza mazungumzo.

    “Kuna nini tena?” akamuuliza Madam S

    “Tumepewa kazi ya kumtafuta Yaumi, kwa maana ametekwa na watu wasiojulikana, mkuu wan chi ana wasiwasi na hali ya usalama kwa sasa, kama watu wanaweza kuingia gerezani pasipo kujulikana na kumteka mtu ambaye yupo katika kitanzi, yumkini basi kuivamia Ikulu!?” Madam S akacheka baada ya kusema hayo.

    “Vipi ulimwambia kama tunaye?”

    “Hapana, sikumwambia, ila nilimwambia tu kuwa aondoe wasiwasi kwani kila kitu kipo kwenye utaratibu,” Madam S akajibu, akanyanyua glass yake na kupiga funda moja la Kilimanjaro lager, bia ya akina mama, kisha akashusha na kuiweka mezani taratibu, “Niambie, kazi yako unaanzia wapi usiku huu, maana hatutakiwi kuwapa nafasi hawa jamaa,” akauliza.

    “Sasa niko njiani kwenda Buguruni kwa Mnyamani,” kamanda akaeleza.



    “Kuna nini huko?”CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Katika mahojiano yangu na Yaumi, kanitajia mtu mmoja anaitwa Fasendy, anasema mwanadada huyo aliweza kumfafanilia kifungu cha tarakimu alichokuwa ameandikiwa na mumewe kabla ya kufa, sasa kwa jinsi alivyokidadavua ndio kitu kilichonivutia, natamani kuonana nae, bila shaka ana mengi ya kunisaidia,” Kamanda Amata akajibu.

    Madam S alimtazama Amata, kisha akashusha kichwa na kuangalia mezani, “Amata unataka kunambia kuwa Yaumi anafahamiana na Fasendy?”

    “Kwa maelezo yake, ndiyo,” Kamanda akajibu.

    “Amekwambia anaishi huko Buguruni? Ok, kama ni yeye basi ni Yule mwanamke hatari ambaye Chiba alikuonesha picha yake pale ofisini jana,” Madam S akaeleza, Kamanda Amata akashtuka kidogo.

    “Kwa vipi Yule atafahamiana na Yaumi? Hapana itakuwa ni mfanano wa majina tu, kwa kuwa alivyonieleza hapana si Yule,” Amata alionesha uhakika kwa kile anachokiongea.

    “Ok, nenda, ukikutana naye, uje unambie anafananaje,” Madam S alimweleza Amata kisha wakaagana na kupeana mkono wa heri, Kamanda Amata akamalizia bia yake na kuondoka kwa Madam S akiahidi kuleta maelezo usiku huohuo.

    Akiwa katika gari, kwa mwendo wa taratibu alikuwa akiicha barabara ya Ally Hassan Mwinyi na kukunja kushoto kuchukua ile ya Kawawa kuja Magomeni, simu yake ikaita kwa fujo, akainyanyua na kuitazama katika kioo, akaona namba tupu isiyo na jina ianawakawaka, akaiweka chini na kuendelea na safari, mara ya pili na mara ya tatu ile simu iliendelea, akaamua kuipokea.

    “Hello, Jaffary, unaongea na Sina, kutoka Magereza Segerea,” ilikuwa sauti tamu ya kike iliyokuwa ikitekenya masikio ya Kamanda Amata.



    “Sina, habari yako,” akajibu, moja kwa moja alijua kuwa ni Yule dada wa mapokezi katika ile zahanati ya Magereza. Aliyemwachia kadi yake ya namba za simu.

    “Nimekumbuka sasa nikakupigia, uko wapi?” Sina akauliza.

    “Nipo kwenye majukumu ya serikali,” Amata akajibu.

    “Aiiiiii jamani, mpaka sasa, mi nilitaka uje kula huku jioni hii,” Sina alibembeleza. Kamanda Amata alijisikia ganzi kidogo kwa mwaliko huo wa ghafla, lakini afanyeje, alibaki kama mbwa aliyeona Chatu, “Ok, basi nikimaliza nitakupigia, nitakuja usijali,” kamanda alikubali.

    “Asante beibi, mwaaaaa!” Sina alimaliza na kukata simu.

    ‘Wanawake bwana, sasa hata mtu humjui we ushamkaribisha kwako, haya nitaenda nikaone hukohuko,’ Kamanda Amata alikuwa akijiwazia alipokuja kurudisha macho barabarni alikuwa tayari amefika njia panda ya Ilala Boma, akakunja kulia kuja Buguruni.



    §§§§§



    “Haya sasa nataka umpigie simu Yule kijana aliyekupa ile bahasha jana uonane nae hapa, mwambie aje kwani ule mzigo Chilungu hajauchukua,” sajini Magreth alimwambia Yule mhudumu wa Kizota Bar, usiku ule walipokuwa ndio kwanza wametoka kituo cha polisi.

    “Sawa, hamna tabu,” Yule mhudumu akainua simu yake na kupiga zile namba, dakika chache tu akawa kamaliza kuongea na Yule kijana kama alivyoamriwa. Sajini Magreth akaketi kwenye meza iliyopo karibu kabisa na mlango ambapo kila anayeingia alimuona, Yule mhudumu alibaki ndani ya gari hakutakiwa kushuka. Magreth alikuwa amewaweka tayri vijana wake wawili waliokuwa na bastola viunoni mwao ili kumtia nguvuni kijana huyo na kumuunganisha kwenye kesi pamoja na Chilungu.

    Nusu saa baadae Yule kijana akafika pale Kizota, akaegesha gari yake kwa mbwembwe zilezile, muziki mkubwa na makelele kibao, akateremka na kuingia ndani ya wigo wa bar hiyo, moja kwa moja akaiendea kaunta. Magreth alikuwa akimwangalia tu kila afanyalo, alipomkosa anyemhitaji akachukua simu yake na kupiga ile namba huku akitoka nje, alipotoka nje ya ule mlango, Magreth alimfuata nyuma na mbele yake akakutana na wale vijana wawili, wakamzuia, “Upo chini ya ulinzi,” mmoja wao akasema, Yule kijana alishtuka na kugeuka nyuma ili akimbie, akakutana uso kwa uso na Sajini Magreth, “Huna uwezo wa kukimbia, twende kituoni, utajua huko kwa nini tumekukamata. Hakuna ujanja, kimya kimya Yule kijana alichukuliwa na kuingia katika gari aina ya Noah waliyoitumia Magreth na wale vijana wawili kufika hapo.

    Breki ya kwanza ilikuwa katika kituo cha polisi Kimanga, akashushwa pamoja na Yule dada mhudumu wa Kizota, akazungushwa kaunta na kuanza kuhojiwa huku akichukuliwa maelezo. “Unamfahamu huyu dada?” aliulizwa na Magreth.

    “Ndiyo namfahamu,” akajibu.

    “Mara ya mwisho ulimuona wapi?” Magreth akaendelea na maswali.

    “Jana, katika bar ya Kizota palepale mliponikamata,” akajibu bila kupindisha.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Safi, sasa huyu dada anahusishwa na kesi ya mauaji yaliyokwishakutokea na yaliyopangwa kutokea, na katika kumhoji amekutaja wewe kuwa ndiye mpangaji wa mauaji hayo, kweli au si kweli?” swali hilo kutoka kwa Magreth lilimmaliza nguvu kabisa yule kijana, alibakia akitazama juu ya dari kana kwamba huko ndiko kwenye jibu la kumpa Magreth.

    “Samahani,” alijibu huku akitetemeka, “Nimepanga mauaji kivipi?|” alijikaza kuuliza.

    “Jana ulipokwenda pale Kizota Bar ulimpelekea nini huyu dada?” swali la Magreth lilijibu swali la Yule kijana. “Nilimpelekea bahasha,” akajibu.

    “Ndani ilikuwa na nini?” akaulizwa tena.

    “Sijui kilichokuwapo, mi nilikabidhiwa nami nikaileta kama ilivyo tena kufuata maelekezo ya aliyenipa bahasha hiyo,” Yule kijana alieleza kila kitu, afande Magreth alikuwa akimtazama kijana huyo na kuona wazi kuwa hajui kilichokuwamo ndani humo, aliwatazama wale askari wengine wawili mmoja alikuwa akiandika yale majibu aliyokuwa akijibu na mwingine akifuatilia kila kinachoendelea katika mahojiano hayo.

    “Nimefurahi sana kwa kuwa umanijibu bila kunificha, sasa naomba unijibu swali la mwisho japokuwa ni refu kidogo, kisha nitakwambia nini kilikuwa kwenye bahasha, nambie nani alikuwa anakutuma bahasha hizo?” Magerth aliuliza swali ambalo koote alikotoka ndilo hasa alikuwa akilitaka. “Kuna jamaa anitwa Swila, ndiye aliyekuwa akinipa hizo bahasha na hata gari niliyokuwa nayo pale ni yak wake,” akajibu. “Namba zake za simu unazo?” lilikuwa swali la shauku kutoka kwa Magreth.

    “Ndiyo afande,” Yule kijana akajibu na kuanza kumtajia namba hizo, Magreth akaziandika kwenye karatasi na kuzihifadhi.

    “Asante sana, wewe unafaa kuwa polisi jamii, najua hakuna ulilonificha na kama lipo basi litakugharimu sana, sikiliza, sasa utalala hapa na sisi leo mpaka upelelezi utakapokamilika ndipo utaachiwa, kwa maana tunaweza kukuacha sasa halafu maisha yako yakawa hatarini, tunapomhifadhi mtu, si kwamba tunamuonea, sisi kama polisi tuna jukumu la kukulinda wewe mwananchi na mali yako, sasa kwa kesi kama hii, endapo tutakuacha sasa uende nyumbani ni hatari kwa maisha yako, huyu Swila akijua lazima atakuua, hivyo basi utakuwa hapa mpaka tutakapomkamata Swila, sisi shida yetu ni huyu Swila,” Magreth alitumia lugha ya kumfanya kijana huyu awe na amani moyoni.



    “Bingo” Magreth aliwaambia wale askari waliokuwa pamoja naye, baada ya kumuweka lokapu Yule kijana ili kuisaidia polisi. Aliitazama saa yake, ilikuwa tayaru ni inakimbilia saa tano za nne za usiku. “Huyu lazima apatikane usiku huu huu,” mmoja wa wale askari alisisitiza, “Habari ndo hiyo, maana tukimpata huyu ndo hasa tutajua kwa nini walimuua ACP Chonde, huyu ana majibu yote,” walikuwa wakibadilishana mawazo usiku huo wakiwa wameketi katika kibenchi kilicho nje ya kituo hicho, sajini Magreth akiwa pamoja nao alikuwa amenyamaza kimya hachangii lolote lakini alionekana kufikiria kitu. “Nyie wanaume, hivi mnamkumbuka Yaumi?” Magreth aliwauliza wale askari wakati wakiwa pale kwenye benchi. “Si Yule aliyemuua mumewe!” mmoja alijibu, “Vipi bado yupo Uganda? Yule mwanamke Ninja Yule namkubali kwa mambo yake,” mwingine akadakia. “Amenyongwa leo asubuhi,” Magreth akawahabarisha na kuwaacha midomo wazi wale askari wenzake.



    Wakiwa katika mazungumzo mara gari moja Harrier yenye rangi nyeusi ilifika na kuegeshwa mbele kidogo ya kituo hicho, ikazimwa taa. Kutoka kwenye gari hiyo akashuka kijana mmoja nadhifu, aliyevalia suruari nyeusi, shati jeupe lililofunikwa kwa koti jeusi, moja kwa moja aliingia kaunta na sajini Magreth alimfuata huku akiwa kawapa ishara wale vijana waingie pamoja nae.

    “ACP Jaffary, karibu sana Kimanga,” Magreth alimkaribisha Kamanda Amata, Jaffary wa bandia.

    “Ndiyo, najua kama umeniita basi kuna jambo,” Amata aliongeza.

    “Yap, ndiyo, tumepata tunachokitaka,” Sajini Magreth alimueleza Kamanda Amata kila kitu walichokuwa wamekifanya mpaka kumpata Yule kijana na ile namba aliyopewa na Yule kijana. “Anaitwa Swila?” alimalizia Magreth kwa kumpa jina Kamanda Amata. “Swila,” alilirudia hilo jina mara kadhaa, “Ok, sasa inabidi atiwe nguvuni lakini mmejipanga vipi?” Kamanda akawauliza.

    “Niliona nikusubiri afande, ili tuone pamoja,” Magreth alijibu.

    “Ok, nipe hiyo namba, wala asipigiwe lakini muda si mrefu tutajua alipo kisha tumvamie na kumtia mikononi bila jasho ikibidi,” Kamanda Amata akatoa mawazo yake, akaichukua ile namba na kuitia katika simu yake, akairusha kwa Chiba na kumtumia sms ‘Nipe uelekea tafadhali’ kisha akakaa kusubiri. Baada ya dakika chache alipata sms nyingine kutoka kwa Chiba, ‘Ruvuma mpaka Maputo, uwanja wa ndege,’ Kamanda Amata akawaambia Magreth na wenzake na kisha wakajiandaa na wote wakaingia kwenye ile Noah na kuondoka zao.



    Ruvuma mpaka Maputo ni baa ya miaka mingi sana katika eneo la njia panda Uwanja wa ndege, kandokando ya barabara iendayo Kalakata. Ni baa ambayo kila mwisho wa juma bendi mbalimbali zilipenda kupiga muziki wa nyumbani na kuwaburudisha wenyeji na wageni wa maeneo hayo.

    Swila, kama anavyojulikana, kijana matata asiye na mzaha kabisa na maisha, siku hii alikuja kujivinjari pamoja na wasichana wake wawili. Imezoeleka kwa walio wengi kuwa na msichana yaani mpenzi mmoja, lakini kwa Swila haikuwa hivyo, yeye alikuwa na wapenzi wawili ambao walikuwa wakifahamiana vyema, hata wakiwa katika kuvunja amri ya sita, kitandani daima huwa wote wakimpa burudani hiyo ya dhambia kuifanya kwa mwanaume au mwanamke asiye mke au mume wako. Alikuwa ameketi kwenye kiti, mwanamke mmoja huku na mwingine kule, mezani kukiwa kumetapakaa vyupa vya pombe zote unazozijua wewe, lugha iliyokuwa inatawala mezani hapo ni ile ile ya waliovumbua pombe hizo, muziki wa nguvu ulikuwa ukiangushwa na bendi ya Msondo Ngoma, huku watu wengi wakiwa wamejiachia kwa starehe hiyo. Swila alikuwa akiponda raha, hakujua hata nini kinaendelea duniani kwa ajili yake. Mhudumu wa baa alikwenda na kumgusa begani, mara simu yake ikaita, namba hakuijua, Kaiinua akaiweka sikioni, haikuongea, akaishusha chini na kuiweka mezani. Sekunde kumi baadae ikaita tena namba ileile, akatukana tusi la nguoni na kuiweka chini, mara ikaita tena, sasa ikapokelewa, simu ile ikamuamuru atoke nje kwani alikuwa anasubiriwa, ukizingatia sauti iliyotumika ni ya mwanamke, Swila akainuka na kwaambia warembo wake wamsubiri, kisha yeye akatoka nje



    SWILA alimtafuta aliyemwita kwa sekunde chache akamuona, Magreth, aliyevaa kiraia, suruali ya jeans iliyomkamata sawia na kuacha bisto zake zionekane vizuri, fulana nyepesi ya rangi nyekundu iliusitiri mwili wake mtamu kwa kuutazama kwa macho.

    “Ndio msichana, sidhani kama nakufahamu,” Swila alizungumza mbele ya Magreth.

    “Ni sawa hunifahamu, lakini nimepewa namba na mtu wako wa karibu sana, ana shida na anatka umsaidie,” Magreth alijibu.

    “Nani? Mbona mi nina ndugu hapa mjini? Ndugu zangu ni pombe tu,” Swila akajibu kijeuri na kugeuka kuondoka zake kurudi baa.

    “Swila mpenzi!” Magreth aliita. Swila akisimama hasa kwa kusikia kaitwa mpenzi, akaanza kurudi kwa mwendo uleule wa kilevi.

    “We mwanamke nani kakutuma kwangu nambie, au kama huna la kusema twende ukanywe pombe,” Swila aliongea kilevi.

    “Hapana, nimetumwa na mama yako,” Magreth alimwambia Swila huku akiondoka eneo lile na kusogea pembeni ambako vijana wake walikuwa wakisubiri mtu huyo akae kwenye engo nzuri, Swila akmfuata Magreth lakini hakufanikiwa kumfikia kwani alijikuta akitazamana na mdomo wa bastola, “Swila, uko chini ya ulinzi,” Swila alibaki akibabaika hajui la kufanya, mara pingu ikatua mikononi mwake akasukumiwa ndani ya gari.



    §§§§§



    Kamanda Amata aliridhika kwa ushirikiano aliopewa na vijana wa polisi kutoka Kimanga, “Magreth, kazi imeenda poa, nashukuru, sasa naomba msijihusishe tena katika hili ila nitakapowahitaji nitakutaarifu, ili swala litafuatiliwa moja kwa moja kutoka katika kituo ofisi maalum ya usalama ili kuumaliza mtandao huu.” Amata alimwambia Magreth huku akimpa mkono wa shukrani, “Kwa lolote nitafute,” akaongeza wakatia akigeuka kuiendea gari yake.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    KITUO CHA POLISI KATI



    INSPEKTA Simbeye alitulia juu ya kiti chake kama kawaida, akijitahidi kukuna tumbo lake ambalo lilikuwa likiifanya nguo yake ya kipolisi kushindwa kukutana sawasawa. Hali hii ilimfanya mzee huyu wa makamo kutumia mavazi ya nyumbani hata awapo ofisini isipokuwa siku maalum na kwa kazi maalumu. Alimkazia macho Kamanda Amata aliyekuwa ameketi mbele yake, kabla hajasema lolote akaitazama saa yake ya ukutani, ilimwambia kuwa ni saa tano za usiku.

    “Yaani we kijana, mi nataka kutoka usiku sasa na wewe ndio unakuja, kuna nini? Au bibi yako Yule kakutuma? Maana ninyi hamuishiwi hoja kama Ukawa,” Simbeye alimtania Kamanda Amata.

    “Ni kweli, usiku sasa hata mimi nilikuwa nataka nikalale kwa kimada, sikia mzee kuna mambo mawili, nadhani kwa vyovyote yatakusisimua nikikwambia, moja mauaji ya ACP Chonde,” Simbeye alimkazia macho Amata kwa hilo alilosikia, “Enhe na la pili,” Simbeye alitega sikio.

    “La pili ni utowekaji wa Yaumi gerezani siku ya utekelezaji wa hukumu yake, najua vijana wako wanahangaika kumtafuta aliyetekeleza huo mpango, usijali waambie warudi, nimekuletea watu watatu ambao ukiwabana watakupa majibu,” Kamanda Amata aliinuka na kumpa ishara ya kumfuta, Simbeye alikiacha kiti chake, mguu kwa mguu mpaka kwenye chumba kimoja kilichofungwa kwa mlango wa vyuma, “Unawaona wale?” Kamanda Amata akauliza, Inspekta Simbeye akajibu kwa kutikisa kichwa, ndani ya mioyo yao kuna unayoyahitaji, mi nimemaliza, nitakuja kesho.

    “Kamanda mbona unaongea mambo nusunusu?” Inspekta Simbeye alikmuuliza Kamnda Amata wakati alipokuwa akiondoka.

    “Hao, ndio waliomuua ACP Chonde na wao ndio wanaojua mpango wa kutoroshwa kwa Yaumi,” ijapokuwa maelezo hayo yalikuwa nusu kweli na nusu si kweli, kamanda Amata aliaga na kuahidi kurudi siku inayofuata.



    Akiwa ndani ya gari yake tayari kwa kuondoka alitazama ile kopi ya hundi aliyoichukua kwenye ile bahasha, ijapokuwa alikuwa na uhakika baada ya kupata majibu ya benki husika kuwa kitabu kile kinamilikiwa na nani, ilikuwa haingii akilini kwa mtu mkubwa kama huyo serikalini kuweza kufanya mambo hayo, kuwalipa wauaji na kupoteza maisha ya watu wanaotegemewa na jamii, akajiuliza kama huyo aliyeuawa, Chonde ndio pekee na Omongwe alipangwa kufuatia au kuna wengine wengi walishapoteza maisha? Hakupata jibu. ‘Chilungu ndiye muuaji, Yule kijana ni tarishi, Swila ndiye mtoa maagizo,’ akatafakari kidogo, ‘Kama ni kampuni ya mauaji basi lazima kuna mkurugenzi au meneja kabisa, sasa ni nani? Labda anayetoa hundi ni mhasibu halafu juu yake ndio kuna wadosi, wanaajiri wauaji?’ Amata akajiuliza lakini hakupata jibu. Kichwa kilimzunguka, akatazama hili na lile kwa makini akajaribu kuhusianisha kisa cha Yaumi na hawa aliowakamata kama kuna muunganiko Fulani, akapata jibu, jibu sahihi, kwenda benki kutazama akaunti ya Chilungu au kama Chilungu alitoa pesa kabla ya kifo cha Chonde aione nakala ya hundi kama muandiko na saini ni ya mtu mmoja na huyu aliyetoa hundi ya kuuawa Omongwe kisha ajue kwanini Omongwe, kwa nini Chonde wakati wao wote walikuwa wakitekeleza majukumu ya kitaifa, na huyu mdosi, mtu mkubwa anayetoa mapesa kununua roho za binadamu amfuatilie pia ili kujua, hakika Kamanda Amata alijikuta kwenya wakati mgumu, ‘Wakinijua wataniua, lakini kufanimeshazoea, nimeshakufa mara kadhaa kwa nini niogope sasa, nitawatia mkononi, nitawaumbua, na lazima nijue siri iliyopo,’ Kamanda Amata akapata nguvu mpya, kama kawaida yake damu ya mwili ikaanza kuchemka, akang’amua kuwa ili akamilishe kazi kwa ufasaha ni lazima atue Kampala, Yaumi alifuata nini Kampala? Ni swali ambalo aliona wazi kuwa jibu lake kwa vyovyote litampa mwanga mpya. Akainua simu yake akabofya namba Fulani akaweka sikioni.



    “Hello Gina, umelala? Wenzako tupo kazini we unalala, motto una raha wewe,” kamanda Amata aliongea kwa sauti ya tuo.

    “Ok, nambie kuna shida yoyote?” Gina alimwuliza Kamanda.

    “Mbona una haraka au umelaliwa?”

    “Unanianza, anilalie nani wakati we unanichunga kama kuku?” Gina alilalama

    “Haya bwana, naomba niandalie safari ya watu wawili kwenda Kampala kesho tafadhali,” Kamanda alimwambia Gina.

    “Vipi, kumekucha?” Gina akauliza kw kupitia simu hiyo.

    “Tena na makucha yake,” Kamanda akamaliza na kuagana na Gina, akamuaga na kusubiri jibu la kazi aliyompa.

    Kwa mwendo wa taratibu akaliondoa gari lake na kuchukua barabara ya Railway mpaka mnara wa saa kisha akanyoosha barabara ya Uhuru na kupotelea pande za Buguruni.



    BGN/MNI 612 B, Kamanda Amata akashusha uso wake baada ya kuisoma namba hiyo na kuhakikisha ni sahihi na ile aliyopewa na Yaumi, nyumba mbovumbovu tu ambayo haikuwa na utaratibu maalum. Ilikuwa saa saba usiku lakini palionekana watu bado wakiingia na kutoka japo mmoja mmoja, ‘Dangulo’ alijiwazia Kamanda, alibaki ndani ya gari yake palepale kwenye maegesho ya klabu ya usiku, na nyumba anayoita ikiwa mbele yake kama mita mia tatu hivi, kwa kutumia darubini yake maalum aliweza kuona kila kitu hata kama ni giza, aliweza kusoma namba za nyumba hiyo zilizoandikwa kwa rangi nyeupe juu ya muimo wa mlango, watu wakiingia na kutoka. Alipojiridhisha kwa hilo akateremka na kujiweka tayari, bastola zake mbili huku na huku, akavuta hatua fupifupi kuelekea katika nyumba hiyo mbovu, akazikwea ngazi zake na kuufikia mlango, akausukuma ukasukumika, akajitoma ndani, kwenye korido ndefu alikutana na wanadada wawili ambao walikuwa wamevaa kiajabu ajabu, walivalia bikini tu na hawakuwa na vazi linguine mwilini mwao, mmoja akamfuata Kamanda na kumkaribisha, “Karibu mgeni, tena we mgeni kwelikweli, hujawahi kuonekana,” yule mwanadada alimwambia Kamnda huku akimpapasa mashavuni na kumtupia busu la shavu, akijigeuzageuza kwa namna ya kutamanisha.



    “Boss wenu yupo?” Kamanda akauliza.

    “Boss, ndo nani, we seme uhudumiwe nini, ila boss hapa hakuna kila mtu ana idara yake,” Yule mwanadada akajibu huku akimpulizia moshi wa sigara usoni.

    “Fasendy!” akatamka.

    “Uuuuuuuhhhhh, Fasendy, utamuweza wewe Yule mwanamke, una pesa wewe?” Yule mwanadada alimwuliza kwa kejeli huku akimuoneshea ishara ya pesa kwa kutumia vidole vyake.

    “Pesa!? Dola, Yuro, Yen, Dinari, Shilingi, Paund, Lira au hela gani mnazungumzia, hapa kila hela inapatikana,” Kamanda alijibu kwa nyodo.

    “Dolari bebi, unamtaka kwa masaa mangapi, ila ni kiziwi Yule anaongea kwa alama, lakini ukimwandikia anasoma?” aliambiwa na kupewa maelekezo kwa huduma hiyo. Kamanda Amata alisikiliza kwa makini na kujikuta hana jinsi isipokuwa ni kukubali kuwa anataka kulala na Fasendy ili ikiwezekana amuone hata akiwa hana nguo kama ni kweli ndiye Yule anayesemwa na Madam S.

    “Masaa mawili yanatosha, nimepata sifa zake kutoka kwa mmoja wa rafiki zangu ambaye amashawahi kulala nae mara kadhaa,” Kamanda alijieleza, kisha akaitwa kwa ndani, akamfuata Yule mwanadada. Walifika kwenye korido ya pili ambako kulikuwa na milango mitatu, kushoto, kulia, na mbele, Yule mdada akafungua ule wa kushoto kwa jinsi ya ajabu, ukafunguka, Kamanda akaingia na kujikuta kwenye sebule ya kisasa kuliko nyumba yenyewe jinsi ilivyo kwa nje, akili ikamcheza kwa haraka, kwa nini nyumba hii ijengwe namna hiyo, aliamini kipo kitu.

    “Karibu!” ilikuwa sauti ya Yule mwanadada ikimkaribisha ndani, Kamanda akaingia na kutazama zile samani zilizowekwa kwa mpangilio, meza kubwa ya kioo iliyotenganisha makochi ya upande mmoja na mwingine, kabati la maana, na luninga ya inchi 110 ilikuwa imetulia ukutani kiasi kwamba wewe unayetazama unajikuta kama ni mmoja wa wanaoonekana ndani ya kioo hicho. Akakribishwa kochi mojawapo kwa kuoneshwa ishara lakini Amata aliketi kwenye kochi linguine, Yule mwanadada akasonya.

    “Fasendy!” Kamanda akatamka tena.

    “Huwezi kumuona kama hujajieleza vya kutosha,” Yule mwanadada aliendelea kuweka vikwazo.

    “Mwambie kaka yake na Yaumi amekuja,” Yule mwanadada akashtuka kidogo kusikia jina hilo likitamkwa. Akainua kidubwasha Fulani kama simu na kubonya vitufe Fulani kisha yeye akaondoka katika chumba hicho. Kamanda Amata, akaingiza mkono katika koti lake na kuiweka sawa bastola yake maana alijua kuwa hapo kuna shari.



    §§§§§CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    USO wa kutisha wa Matinya ulionekana wazi usiku huo baada ya kuambiwa kuwa vibaraka wao waliokuwa wakitumwa kutekeleza mauaji wametiwa mbaroni. Lakini alijipa matumaini ya kutoweza kugundulika mpango wao huo.

    “Sikia Scogon, kwani ulivyokuwa unampa hizo hundi mlionana wakati wowote?” Matinya aliuliza.

    “Hapana, mimi ni profesheno boss, nilikuwa namuwekea palepale juu ya kaburi na kumpa maelekezo, hatukuwahi kuonana,” Scogon akajibu.

    “Vizuri, ndio maana nilikupa ukamanda, sasa wale vijana nitajua cha kufanya, ila lazima wapotelee hukohuko lupango lazima uandaliwe mpango wauawe ijapokuwa najua kuwa hawawezi kutugusa kwa lolote,” Matinya alizungumza, akainua glass yake na kujimiminia pombe iliyobaki, “Keshokutwa lile kontena litatoka na kuondoka mara moja, wewe na Fasendy ambaye ndiye mkufunzi wa mafunzo mtafuatana nalo na mara moja mtaanzisha mafunzo kule msituni, tunamwezi mmoja tu wa kutekeleza lile tulilolipanga”. Scogon alitafakari kwa sekunde kadhaa, akajaribu kukumbuka kama kuna wakati wowote alioweza kugongana sura na Swila, hakuna, hakukumbuka chochote, kwa maana alijua kama wanakamatwa kwa kufutana, nani baada ya nani basi sasa ni zamu yake, alikumbuka jinsi alivyompa ile bahasha usiku wa manane. Makaburi ya Kinondoni, katikati aliiweka ile bahasha juu ya kaburi mojawapo na kisha kuondoka eneo lile, akatulia sehemu kusubiri kama mpango umesukika, baada ya lisaa limoja, saa tisa ya usiku, Swila alifika eneo lile, Scogon alimuona vizuri sana, mpaka alipokwenda na kuichukua ile bahasha, mission clear.



    Akiwa kwenye kochi kubwa la vono, Scogon aliingiwa na kibaridi cha faraja kuwa hakuwa na mkutano wowote wa uso kwa uso na Swila. Alipokumbuka mara ya pili napo ilikuwavivyohivyo, akajihakikishia kama ni kutaja aliyewatuma basi angetaja kaburi, kama ni simu ilishateketezwa kwa moto kitambo kirefu sana, na simu ya mwito wa kwanza na ile ya mwito wa pili zilipigwa kwa namba tofauti, muelekeo tofauti, na eneo la tukio ni tofauti, kisha nayo ikateketezwa, zote zilifichwa namba. ‘Hamna kitu,’

    “Sasa sikiliza, katika jeshi la polisi kituo cha kati hakuna mtu anyeitwa Jaffari na kwa cheo hicho, hivyo hapo lazima kuna mchezo tumechezewa, Bwana Gomegwa akishatoa lile kontena, hatakiwi kuishi maana atakuwa amejua kipande cha siri yetu” Matinya aliendelea kutoa maelekezo, “Ninachotaka sasa, ni ulinzi mkali kila mahali, muwekee mtu Omongwe, huyu Magreth najua mimi la kufanya yeye hawezi kuniumiza kichwa kwani yuko chini ya idara yangu,”





    “Sawa boss,” Scogon alijibu. Matinya alimuaga kijana wake huyo na kuelekea chumbani ambako alimuacha afande Marina. Alipofika alimkuta amekwishalala muda mrefu, akamtazama na kusonya kisha akapunguza mavazi aliyoyavaa mwilini na kujiandaa kupanda kitandani, lakini kabla hajafanya lolote simu yake iliita, akaitazama, namba iliyokuwa ikionekana aliijua vyema, ‘Simbeye,’ alijisemea moyoni.

    Gabriel Matinya alikuwa akimfahamu sana Inspekta Simbeye kwa uhodari katika kazi yake ijapokuwa alikuwa na mwili mkubwa uliojaa mafuta, aliitazama tena ile simu akajishauri kama anaweza kuipokea au la, baada ya mapambannnaaao makali nafsini mwake aliamua kuipoka simu hiyo.

    “Ndiyo Inspekta!” Matinya aliitikia huku akisikiliza kwa makini.

    “Nafikiri hili linakuhusu kwa namna moja au nyingine,” Simbeye aliongea kwa mtindo huo kama kawaida yake.

    “Niambie Inspekta,” Matinya alitoa ombi.



    “Nina watu watatu hapa chini ya ulinzi, nimewahoji vya kutosha ndiyo wanaohusika na mauji ya kijana wetu Chonde, naomba uje hapa asubuhi wewe mwenyewe utajua,” Inspekta alimaliza.

    “Nimekusoma Inspekta,” Matinya alijibu na kujitupa kitandani, akashusha pumzi ndefu, mawazo yakamtawala. ‘Ananiita nikawaone watu hao au wamekwishaniweka kwenye orodha ya washukiwa? Lo kitumbua kimeingia mchanga,’ alijiwazia na kujikuta akiwa na jasho mwili mzima, Marina aliamka katikati ya usiku, na kuanza kumpapasa Matinya juu ya tumbo lake hasa zaidi chini ya kitovu, Matinya aliusukuma mkono wa Marina.

    “Bebi vipi jamani, mbona siku hizi umebadilika?” Marina alilalama.

    “Kuna wakati wa mapenzi na wakati wa kazi,” Matinya alijibu.

    Baada ya kusema hayo akaingia kwenye shuka na kugeukia upande mwingine akimwacha Marina na maswali kichwani.



    §§§§§



    KAMANDA Amata alitulia tuli, sasa akiwa peke yake pale sebuleni ijapokuwa yeye mwenyewe alijua wazi kuwa sehemu kama hiyo huwezi kuwa peke yako, alitulia huku mkono wake bado ukiwa ndani ya koti lake tayari kwa lolote litakalojiri katika eneo hilo. Bado akiwa katika kutafakari ndipo alipoona sehemu Fulani ya ukuta huo ambayo ilikuwa na picha kubwa ya mwanadada wa kizungu aliyesimama kwa mtindo wa pekee tena isitoshe alikuwa kama alivyozaliwa, ‘Dlimwengu wa kibepari huu’ alijiwazia wakati ile picha ikionekana kama inageuka kupotelea kwa ndani, na ghafla msichana mrefu kiasi ilikuwa tabu kujua kama ni mnene au mwembamba kutokana na vazi alilokuwa amelivaa lililomfunika kila sehemu ya mwili wake isipokuwa macho tu. Aliketi katika kiti cha mbele yake huku akimtazama Kamanda Amata aliyekuwa pale sebuleni jinsi alivyokuwa akimshangaa mwanadada huyo.

    “Karibu sana mgeni, unataka huduma ya falagha na mimi?” akauliza Fasendy.

    “Hapana, nimekuja kufuata mzigo ambao shoga yako yaumi alikuwa ameuacha hapa,” Kamanda Amata alimueleza.

    “Ok wewe ni nani?” Fasendy akauliza.

    “Bwana wake wa pembeni, ni jana tu nilipowasiliana nye nay eye kunipa maagizo haya pamoja na namba ya nyumba hii,” Kamanda akajieleza.



    “Ok, Yaumi ni rafiki yangu sana, ni kweli kuna mzigo aliuacha hapa siku nyingi nyuma kabla hayajatokea yale ya Kampala, sasa hebu nambie yuko wapi? Maana nilisikia kuwa ametekwa siku ya kunyongwa kwake,” Fasendy aliendelea kuzungumza kwa kuchanganya lugha ya alama za viziwi pamoja na maneno ambayo alitamka kwa shida kidogo na kwa mtindo wa pekee kana kwamba alikuwa ni motto anayejifunza kuongea.

    “Yupo, kwa sasa tumemficha huko katika misitu ya Kazimzumbwi, na keshokutwa alfajiri ataondoka nchini kwa njia ya barabara mpaka Lusaka ambako atachukua ndege na kuelekea USA kupumzika maisha yake yote.

    “Ok, nimefurahi kwa hilo, maana nilisikia kwenye vyombo vya habari juu kupotea kwake,” aliposema hayo akanyanyuka na kupita palepale kisha akarudii na mfuko wa plastiki uliokuwa na vitu kadhaa ndani yake, Kamanda akaupokea na kutoka pale alipoketi, aliupekuwa mfuko huo harakaharaka akaona nguo chache, za nje na za ndani, wallet moja ya kiume, hakukuwa na kitu kingine zaidi.

    “Ni hivi tu?” akauliza.

    “Ndiyo hakuna cha zaidi, msalimie sana mwambie namuombea heri katika yote lakini akiwa ametulia anitafute kwa simu” Fasendy alimwambia Kamanda wakati huo alikuwa tayari amesimama.

    “Sawa zimefika, na nitahakikisha anakutafuta kabla hajaondoka, maana hata yeye anakutafuta sana,” Amata aliongeza.

    “Oh, samahani, si vibaya kama ningekujua jina lako,” lilikuwa ni ombi kutoka kwa Fasendy kwenda kwa Kamanda Amata.

    “Jaffari,” alijibu kwa haraka huku akimpa mkono Fasendy kwa kuagana naye. Kamanda Amata alikutana na kiganja kikavu cha mwanadada huyo na kwa harakaharaka aligundua kuwa mkono huo si bure ila unaonekana kuwa na shuruba nyingi.



    Akiwa kwenye gari yake, Kamanda Amata alikuwa na mawazo lukuki juu ya shughuli hiyo inayomkabili ambayo sasa alishaona kuwa uzito wake ni mkubwa, akajiuliza sana juu ya nyumba hiyo ya Fasendy kwa jinsi ilivyo nje na ndani, akilini mwake alijua wazi kuwa lazima kuna kitu zaidi ya nyumba ya kawaida. CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Breki zake zilifanya kazi na kusimamisha gari hiyo pembezoni mwa mtaa Fulani huko Kimanga, ukimya uliotawala eneo lote hilo ulimfanya kamanda Amata kuchukua tahadhali hasa wapi pa kuliacha gari lake, alizungusha huku na kule na mahali Fulani alikuta kuna kagiza kidogo maana palikuwa pamefunikwa na miembe miwili mikubwa iliyokuwa upande mmoja na mwingine wa barabara, akaegesha hapo na kuzima gari kisha akatulia kama dakika kumi hivi, hakuona dalili zozote za mtu eneo hilo zaidi ya mbwa waliokuwa wakirandaranda huku na kule. Akashuka na kuuurudishia mlango kabla ya kuufunga kwa rimoti maalum ya gari hiyo.

    Kisha akiwa ameweka mikono yake katika mifuko ya koti lake upande huu na ule alitembea taratibu akipita upenuni mwa nyumba hizo, huku akimulikwa na taa za nje za majumba hayo ambayo ndani yake watu walikuwa wamelala fofofo hawajui ulimwengiu wa ulikuwa ukikabiliwa na vitu gani. Aliifikia nyumba anayoitaka, nyumba ya iliyokuwa ikikaliwa na Yaumi na bwana Kajiba kabla ya umauti wake. Alizunguka upande wa nyuma ambapo palitawaliwa na zao la matembele alitazama pande zote hakuona tatizo, kwa sekunde mbili aliukwea ukuta huo na ile ya tatu ilimkuta akitua taratibu kwenye uwa wa nyumba hiyo, akatembea kwa hatua za tahadhari mapaka kwenye mlango wan a kuuchezea kidogo tu nao ukamchekea, akaingia ndani kufuata kijikorido kifupi kabla hajafika sebuleni ambako alikukuta kupo katika hali ya usafi kana kwamba kulikuwa na mtu anayeishi katika nyumba hiyo, alirudi kinyumenyume mpaka kwenye mlango mmoja wapo ulioonekana wazi kuwa ndiyo ‘Master Bedroom,’ akauchezea vile vile na kuingia ndani kisha akajifungia, kwa kusaidiwa na mwanga mkali ila usiotawanyika mbali wa kurunzi yake ndogo mithili ya kalamu aliweza kuona hapa na pale.



    Akaiendea droo ya kitanda na kupekuapekua hakuona kama kuna analolihitaji, droo zote za kabati bado hakuona kama kuna la maana kwake. Dakika tano alizitumia ndani ya ndani ya chumba hicho akipekuwa huku na kule lakini tayari sehemu zote zilikwishapekuliwa na Yaumi na wabaya wake hivyo kila kilicho cha muhimu kama si Yaumi basi wale watu walikwishakuchukua. Kamanda Amata akaona hakuna haja ya kupoteza muda katika nyumba hiyo, akavuta hatua chache kuuelekea mlango, kabla hajaufungua, akili yake ilizungumza kitu, akageuka nyuma na macho yake yakakutana na picha kubwa ukutani, picha ya kioo safi, aliweza kuiona kwa kutumia ule mwanga wa ile kurunzi, akaitilia shaka picha hiyo, akaiendea na kusimama mbele yake, mara hii alizima ile kurunzi, akatoa miwani yake maalumu ya kuweza kuona gizani akaipachika usoni mwake, naam aliweza kuona sawia, akapapasa ile picha kana kwamba anataka kuiondoa pale ilipo, katika moja ya vipepeo ambao walikuwa kwenye picha hiyo hakuwa kipepeo wa kawaida, Kamanda Amata alimgundua Yule kipepeo, kipepeo hadimu sana duniani anayepatikana katika nchi ya Tanzania pekee huko Udzungwa katika milima ya tao la Mashariki. Kati ya vipepeo wengi walioipamba picha hiyo, ni huyo tu aliyemvuti Amata, kwa wepesi wa akili na kazi yake, aligundua kuwa hakuwa kipepeo wa kawaida akmgusagusa kwa namna Fulani hivi kwa mtindo tofauti, mtindo wa tano ulikuwa ni sahihi kabisa, ile picha ikafunguka kama kajimlango kadogo na kuruhusu Kamanda Amata akutane na lock ya kielektroniki iliyofunga eneo hilo kwa ndani, ‘Bingo!’ kwa kuwa lock hiyo ilikuwa ikifunguliwa kwa namba maalumu, Kamanda Amata alikuwa na mchanganyo wa namba niyingine, tarakimu 12 ambazo si rahisi kwa binadamu wa kawaida kuzijua, akaziingiza katika kile kibompoli chenye tarakimu 9 na mara kitu kama droo ya sefu ikafunguka kwa kutokeza kwa nje taratibu. Ndani ya droo hiyo kulikuwa na makabrasha kadhaa, hakuna muda wa kuyasoma, Kamanda Amata akayanyanyua kama yalivyo na kuyaweka juu ya kitanda, akachuku karatasi kutoka mfukoni mwake na kuandika ujumbe Fulani kisha akaitumbukiza katika droo ile na kuifunga kama ilivyokuwa, akavua koti lake na kukusanyia vile vikolokolo na makabrasha Fulani na baadhi zilikuwa ni pesa taslimu akarundika yote katika koti lake na kutoka eneo hilo bila kujulikana na mtu.



    §§§§§



    Pambazuko la siku iliyfuata lilimkuta Matinya katika VX lake la serikali akiingia mijini kutoka nyumbani kwake, yeye hakubanwa na foleni kwani hata hao wanaoruhusu fokeni ni vijana wake, moja kwa moja alifika katika jengo ilipo ofisi yake, wizara ya mambo ya ndani ya nchi. Bila kuchelewa aliendea daftari maalum na kuweka saini akifuatiwa na wengine wa chini yake kicheo. Kisha akarudi garini.

    “Twende kituo cha polisi kati mara moja,” alimuamuru dereva na safari ikaanza. Haikuwachuku muda mrefu tayari walikuwa katika kituo hicho, salamu za utii kwa mkubwa, salamu za kijeshi zilimwagika kwa Matinya amabye mkononi mwake alishika rediocall yake. Alikuwa akitembea harakaharaka mpaka kwenye ofisi ya Inspekta Simbeye, bila kugonga hodi aliingia na kumkuta mzee huyo aliyechoka kinamna Fulani.

    Inspekta Simbeye alimkaribisha Matinya na kuketi naye wakiwa wanatazamana.

    “Ndiyo Inspekta nimeitikia wito wako,” Matinya alianzisha mazungumzo.

    “Nami nashukuru, hapa kuna vijana watatu wameletwa jana kutoka kituo cha polisi cha Tabata na Kimanga, wameletwa kwa tuhumu za kufanya mauaji ya ACP Chonde, baada ya kuwabana sana kwa kipigo kinachostahili, mmoja wao akaropoka kama si kusema kuwa pia alishiriki katika mauaji ya Bwana kajiba kule Kimanga kwa kuwa yeye huwa anakodiwa tu kwa kazi hiyo kwa malipo maalum. Kwa kuwa swala la mauaji ya Kajiba lilikuwa katika idara nyeti ya polisi ambayo inapata maelekezo kutoka kwako, ndio maana nikakuita uusikie utata huu wewe mwenyewe. Ni kweli anayosema kijana huyu au ni vinginevyo?” Simbeye akawasha mtambo maalumu wenye kunasa sauti, akazirudia sauti za mahojiano na kijana Yule, Matinya alisikia wazi yaliyokuwa yanasemwa na kijana huyo, mshtuko wa wazi ulionekana machoni mwa Matinya, akajua lol, sasa siri inafichuka, ‘Swila!’ akatamka jina hilo moyoni mwake kwa hasira.

    “Inspekta Simbeye, umefanya kazi kubwa ambayo ilikuwa inatutia utata na kutunyima usingizi, tulimhukumu Yule mwanamama bila kosa!” Matinya akajifanya anasikitika lakini halikuwa sikitiko la kutoka moyoni, kisha akamtazama Simbeye, “Ok, hilo liache maadam liko chini yangu nitawapa kazi wale vijana waje kumshughulikia ili aseme na wenzake wote kisha tujue tunafanya nini,” akamwambia Inspekta Simbeye kisha akaondoka zake huku akimwagiwa saluti za kutosha.



    Ndani ya ofisi yake alikuwa mara ashike hiki mara kile ilimradi tu alikosa utulivu, nafsini mwake ilikuwa ni pigo kubwa sana kwa hatua hiyo ya mtu kujitaja kuwa ameshiriki mauaji ya Kajiba, hakutegemea lakini sasa aligundua kosa alilolifanya…





    *************

    *******************

    **********************



    Kamanda Amata alitoa tabasamu pana kwa Madam S kwa kusikia kauli hiyo.

    “Mi Mlokole Madam!” kamanda alitania.

    “Ungekuwa we ni mlokole serikalim ingefunga hilo kanisa maana lingekuwa la wakengeufu, nenda zako bwana mi nina shughuli zangu,” Madam S alimwambia Kamanda.

    Kamanda Amata alitoka ofisini kwa Madam S na kupanda pikipiki lake akielekea nuwanja wa ndege, ijapokuwa kulikuwa na foleni lakini aliweza kupenya hapa na pale na akafika mapema. Ilikuwa bado saa moja ndege iondoke, aliacha pikipiki yake na kuingia ndani, moja kwa moja akapita mpaka sehemu ya kuondokea abiria kwa kuwa daima alikuwa hakaguliwi.

    “Chiba!” aliita Kamanda alipokuwa nyuma yake.

    “Oh Kamanda, mtu wetu huyu hapa,” Chiba alimwambia Kamanda huku akimuonesha kwa mwanadada aliyevalia guo kubwa jeusi, lililoruhusu macho tu kuonekana.

    “Ok, Chiba, kuna kazi nyingine, nataka unifanyie uchambuzi wa namba Fulani kasha unitumie haraka, ukitoka hapa nenda kwa Madam S atakuonesha,” Kamanda alitoa maelekezo, akaagana na Chiba.

    “Beibi,” Kamanda aliita.

    “Beibi,” Yaumi alijibu. Kamanda Amata akainuka na kumshika mkono wakaondoka na kuingia chumba kingine, wakaketi humo.

    “Yaumi, tunaenda Kampala, nina uhakika ulikuwa sahihi kwenda Kampala, twende ntukaona kuna nini ili tupate jibu la kitendawili hiki, nikuulize swali?” Kamanda alimuongelesha Yaumi.

    “Sema au uliza,” Yaumi akajibu kwa sauti ya chini.

    “Unajua lolote katika juu ya namba hii?” akamtajiia ile namba aliyoipaya katika kile kitabu. Yaumi alitulia kimya kwa muda akiitazama ile namba,

    “Tarakimu nne za mwisho nakumbuka alikuwa anapenda sana kuzitumia kwenye simu yake kuhifadhi kumbukumbu,” Yaumi alijibu. Kamanda Amata aligwaya kwa jibu hilo, alitulia kufikiri juu ya jibu hilo,

    “Niambie, kivipi?” kamanda aliuliza.

    “Alikuwa na simu ambayo akibofya namba hizo aliweza kurekodi ujumbe wowote autakao, lakini sikumbuki alikuwa anabonyeza vipi, kuna jinsi alikuwa akifanya,” Yaumi alijibu. Kamanda Amata akachukua simu yake na kumtumia meseji hiyo Chiba ili naye aweze kufanya lolote katika hilo. Tangazo la kuwataka abiria waingie ndegeni likasikika, kamanda Amata akamshika mkono Yaumi na wote wawili wakaingia ndegeni tayari kwa safari.



    ******************************



    Sajini Magreth alianza kazi siku hiyohiyo katika ofisi yake mpya. Alipewa maelekezo ya kazi kuwa kila anapokwenda lazima atoe taaridfa kwa IGP ili ijulikane ni wapi alielekea. Kwa ujumla Matinya alitaka kujua nyendo za Margreth ili ajue ni wapi anaweza kuitimiza azma yake.

    Ofisi mpya ilikuwa ngumu sana kwa Sajini Margerth kutokana na kazi nyingi na pia kazi ngumui, kila wakati alijikuta akiwa na kazi ngumu za kuzifanya, ijapokuwa kulikuwa na posho nyingi za hapa na pale lakini bado alikiri kuwa kazi ile ilikuwa ngumu sana. IGP Matinya alifurahi kuona uchapakazi wa Mgreth lakini bado alikuwa akimwangalia ni wakati gani ambao angeweza kumuweka katika kumi na nane zake ili amalize kazi. Matinya alidhamiria kumpoteza Magreth kutokana na kuwa alikuwa tayari anajua mambo mengi sana juu ya kesi hiyo ya Yaumi.



    *****************************************

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    CHIBA na Madam S walikuwa bize kujaribu kufungua fumbo hilo, Chiba alijaribu kila namna ya kutengeneza zile namba ili zilete maana lakini bado ilikuwa ni ngumu, kila akizigeuza kwa mtindo huu au ule bado hazikuleta maana. Walibaki hoi, ‘Marehemu katuweza’ Chiba alijiwazia. Madam S alibaki kimya kumtazama.

    “Chiba, vipi, ujanja leo umekuishia?” Madam S alimtania Chiba aliyekuwa akitembea huku na huku ndani ya ofisi hiyo, “Lakini si mwenyewe si amesema kuwa hizo tarakimu nne za mwisho ni namba za kufungulia begi la mumewe, sasa we unachohangaika ni nini?” madam S aliongeza.

    “Hata kama, hilo begi liko wapi?” Chiba aliuliza huku bado akiendelea kuzunguka zunguka, “Na nakuambia nikipata maana ya namba hii kazi imekwisha,” Chiba alijitupa kwenye moja ya makochi yaliyopangwa vizuri kabisa katika ofisi hiyo, akitafakari jambo moja au mawili kwa kina.

    0013205 Chiba aliendelea kuitazama namba ile huku akiendelea kujartibu kuichezea angalau impe maana fulani.

    Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Kampala

    YAPATA saa kumi jioni ndege iliyowabeba Kamanda Amata na Yaumi ilifika Kampala. Kwakuwa hawakuwa na mizigo ilikuwa ni muda mchache kutoka ndani na kuelekea barabarani, walifika na mara moja wakaingia kwenye tax,

    “Protea Hotel tafadhali” Kamanda Amata alimweleza dereva wa tax na safari ikaanza, mitaa michache ilimfanya dereva afanye kazi ya ziada ili kuwawahisha wageni wake. Kutokana na ujuaji wa mji walifika bila kuchelewa, Amata akamlipa pesa Yule kijana kasha akaielekea kauntaaaaa tayari kuchukua chumba chake. Kitanda kikubwa kiliwalaki wageni hao, nao bila hiyana wakawa kama wamefika nyumbani. Kamanda Amata alikiendea kiti kilicho pembeni kabisa ya chumba hicho, kutoka kwenye jokofu akajitwalia kinywa akipendacho na kuketi kitini huku bastola zake mbili akiwa amezining’iniza kwenye mikanda maalumu aliyoivaa ndani ya koti lake.

    Yaumi yeye alijitupa kitandani, na mjitupo huo ulimfanya mwili wake kujichora vizuri na kumshawishi Kamanda Amata. Kamanda alimtazama Yule mwanadada kwa tuo, kiroho kikimdunda. ‘Ushindwe shetani!’ alijisemea wakati akikunja nne kwenye kiti ambacho mbele yake kulikuwa na meza iliyokwisha wekwa mvinyo. Aliichukua kile kitabu cha kumbukumbu na kuendelea kukipekua pekua ili aone kama kuna linguine. Katika kurasa za mbele kabisa alikutana na kumbukumbu nyingine lakini hazikuwa na msaada sana, Kamanda Amata alifikiri sana juu ya nini la kufanya huko Kampala, kila nukta iliyokuwa ikipita katika saa yake alikuwa anionea uchungu. Akaamka na kumfata Yaumi pale kitandani, akamsukasuka kumuamsha maana tayari alikuwa akikoroma, Yaumi aliamka kwa tabu kidogo, jicho lake aklipeleka katika saa ya ukutani, tayari ilikuwa saa kumi na mbili kasororobo jioni.



    “Sasa kuanzia muda huu utaitwa Zaina, na hati yako ya kusafiria imeandikwa jina hilo, hii hapa,” Kamanda alimjuza Yaumi jina hilo jipya na kumpa ile hati ya kusafiria iliyotengenezwa ndani ya lisaa limoja huko Dar es salaam, “Ijapokuwa hakuna anayejua ujio wetu hapa Kampala lakini lazima tuwe na tahadhari ya hali ya juu sana, hakikisha unavaa ile barakoa yako ili usijulikane,” Amata aliendelea kutoa maelekezo.

    “Barakoa?” Yaumi aliuliza.

    “Ndiyo, mask, yaani kukaa kote Dar hujui Kiswahili, utaivaa ili ikupe sura nyingine na sasa utavaa suruali na fulana amabzo ziyakupa urahisi wa kutembea au kukimbia inakobidi,” Kamanda akampa hivyo vitu vyote. Yaumi akaingia bafuni kujiandaa, ‘Hii ndo mitego ya Madam S, anajua kabisa mi ni lijali halagfu eti hakikisha humuwachi kila utakapokuwa nay eye awepo, sasa leo tutalalaje humu ndani,’ Amata alijiwazia huku akimtazama Yaumi aliyekuwa akiingia bafuni. Kamanda Amata alikula kwa macho, motto huyo wa kizaramu aliyeumbika vizuri, mfupi wa wastani, kibonge mwenye makalio ya haja, kifua kiichokuwa na matiti yaliyokitosha kwa ukubwa kadiri ya umbo lake. Kamanda Amata aliinua glass yake na kuimiminia mvinyo hiyo kinywani, huku akijiramba kwa ladha safi ya kinywaji hicho. Mara saa yake ikamfinya kwa mbal;I, akajua kuna ujumbe, aliinua mkono na kuiruhusu ilete ujumbe huo.

    ‘…Kamanda Amata, uwe na tahadhari sana, ijapokuwa hakuna anayejua juu ya safari yako lakini wapo, na uangalie sana utembeapo na huyo mrembo. Tunakutumia maana ya zile namba tunaomba uyitumie sawasawa kasha utupe majibu,’

    Mara zilikuja namba tarakimu zilizokuwa na mambo tofauti, namaba ya nyumba, barabara, simu, posta nk. Ilitakiwa Kamanda atumie hizo namba ama kupiga simu au kwenda kwenye namba husika au vyovyote vile. Kamanda Amata alitikisa kichwa na wakati huo tayari Yaumi alijitokeza kutoka bafuni akiwa mwingine kabisa, jeans aliyoivaa ilimpa shepu tofauti kabisa ambayo ilimfanya Amata kukubaliana na kajiba juu ya uchaguzi wa mwanamke huyo, ‘kwa nini watu walitaka kukatisha maisha ya mrembo huyu?’ alijiwazia.



    Simu ya Madam S iliita kwa fujo pale mezani ilipowekwa, ilikuwa ni kitendo cha kuogofya kidogo kwa maana muda huo tayari ilikuwa ofisi zimefungwa, akainua uso wake na kumtazama Chiba aliyekuwa akifanya kazi katika kompyuta yake.

    “Chiba!” akaita.

    “Niambie Madam,” Chiba akajibu.

    “Pokea simu hiyo!” akamwambia, Chiba akamtazama Madam S.

    “Simu yako, mi nitapokeaje?” Chiba akauliza.

    “Aliyepiga anajua kabisa hii ni saa kumi na mbili jioni na hakuna mtu ofisini, ina maana anajua kuwa nipo au mahali anapopiga simu hii ananiona, siku hizi lazima tuishi kwa ujanja na umakini, pokea simu hiyo mwambie mi sipo halafu usikie anasemaje,”

    Chiba kabla ya kuipokea simu ile, akafunmgua mkoba wake na kutoa kitu kama shilingi mia mbili kwa umbo na ukubwa wake, akaiinua ile simu na kwa haraka akakipachika pale pa kusikilizia, kisha akaiweka sikioni,



    “Hallo!” aliita na kutulia kusikiliza sauti ya upande wa pili, hakukuwa na majibu ila alisikika mtu anayehema kwa shida, sauti za kitu kama vurugu kwa mbali, zingine zikipiga mayoe na zingine ni za vitu kama viti kuanguka. Mara kwa shida ilisikika sauti ilioongea kwa mkoromo.

    “Wa .. me .. ni .. ua, nisaidie,” ile sauti ilitoka kwa tabu.

    “Uko wapi na we ni nani?” Chiba aliuliza kwa haraka.

    “Nipo Ki… mar…a S…uk…a!” na zaidi ya hapo haikusikika ile sauti bali kelele za watu waliosikika wakikaribia simu ile.

    Chiba aliendelea kusikilizia lakini alipoona ni kelele za watu kulia, aliiweka simu ile mezani bila kukata, akashusha pumzi.

    “Madam, ilikuwa simu yako? Au imepotea njia?”

    “kama imepigwa hapa nafikiri ilinikusudia mimi, lakini kwa nini asipige polisi? Chiba twende, kasema ni wapi?” Madam alisisitiza, kisha akavuta motto wa meza na kutoa bastola moja, akaifunga kiwambo cha sauti na kuipachika mkobani.



    “Chiba twende, mengine yatajulikana ukohuko,” madama aliongeza msisitizo, Chiba akakunja ile kompyuta na kujiweka tayari wakafunga ofisi na kuiendea gari, “Hapana Madam, ili tuwahi tutumie hii pikipiki ya Kamanda,” akisema hayo Chiba alikuwa tayari amekati juu ya pikipiki hiyo aina ya Cagiva, Madam S akakaa nyuma yake na kumshika vizuri Chiba, “Ole wako uniangushe!” madam alitoa onyo. Kisha safari ikaanza. Mwendo wa pikipiki hiyo uliwafanya hata polisi wa usalama barabarani kutahayari, kwa mwendo uleule iliwachukua dakika kumi na tano tu kuimaliza Ubingo na kuianza Kimara, walipokaribia hoteli ya Mbombeye walipishana na gari ya wagonjwa iliyopita kwa kasi kuelekea mjini.

    “Simama!” Madam alimuamuru Chiba, naye akatii. Chiba akaitoa pikipiki nje ya barabara, Madam akateremka na kuitazama ile gari ya wagonjwa ikipotelea kwenye upeo wa macho yake. Akapanda tena juu ya pikipiki lile na Chiba kwa mwendo wa taratibu akaingia barabara ya vumbi na kuifuata kama anakuja mbezi, akasimama katika kikundi cha watu na kuwauliza kulikoni, ndipo wakapata habari hizo za mshtuko, ilikuwa ni jioni hiyo tukio la mauaji lilitokea katika jumba la jaji Ramson, Chiba hakusubiri habari hiyo ikamilike, akauliza ni wapi nyumba hiyo ilipo akaoneshwa mtaa wa nyuma yake, akaondoa pikipiki lake mpaka katika geti kubwa jeusi ambalo bila shaka ndilo jumba la jaji Ramson, alikaribishwa na vilio na vurugui za hapa na pale. Wakashuka na kuingia ndani ya ua wa jumba hilo, akina mama na akina baba kadhaa walikuwa wakizungumza hili na lile. Mzee mmoja wa makamo aliwakaribisha.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Sisi ni maafisa usalama, tuambieni nini kimetokea?” Chiba alinza mazungumzo namna hiyo huku akionesha kitambulisho bandia cha upolisi.



    “Kijana hapa bwana kumetokea tukio la mauaji, kama dakika ishirini au thelathini zilizopita,” Yule mzee alijibu baada ya kujitambulisha kuwa yeye ndiye balozi wa nyumba kumi.

    “Muuaji mmemuona?” lilikuwa swali la Madam S huku akipanda ngazi kuelekea mlango mkubwa wa nyumba hiyo ya kifahari.

    “Hapana, mkewe alimsikia mumewe akipiga kelele ndipo alipomkimbilia na kumkuta akivuja damu huku akiongea na simu, twendeni muone,” Yule mzee alijibu huku akifuata nyuma ya Madam S na kuingia nao ndani kuangalia eneo la tukio. Damu nzito ilikuwa imetapakaa katika meza ya kulia chakula, kisha matone kiasi kuelekea meza ndogo iliyokuwa na simu TTCL, mkonga wa simu ulikuwa chini, Madam S alitazama eneo lile na kisha akatazama kile kiti ambacho mheshimiwa jaji aliketi akipata chai ya jioni, simu yake ilibaki palepale mezani, Chiba akaichukua na kuitia kwenye mfuko maalumu wa plastiki.

    “Madam, tazama dirishani,” Chiba alimwambia Madam S, alipoinua uso wake alikutana na tundu lenye kipenyo cha kama milimita tano likisindikizwa na nyufa nyembamba kuzunguka tundu hilo.

    “Amedunguliwa!” Madam S alimjibu Chiba huku akibaki mdomo wazi, aligundu kuwa muuaji alifanya shambulio lake kutokea nje, akijuwa wazi kuwa muda huo mlengwa wake ataketi hapo, nje ya dirisha hilo kulikuwa na jengio la ghorofa nne lakini lilikuwa halijaisha bado, lilikuwa gofu lenye manyasi na tando za buibui. Madam S akifuatiwa na Chiba walitoka nje ya nyumba hiyo na kuliendela ghorofa lile bila kusita wala kuuliza walizikwea ngazi mpaka chumba walichokusudia, hakika, kachero ni kachero tu, Madam S alisimama mkabala na Chiba kisha wote wakatazama chini na kuliona ganda la risasi moja tu iliyotosha kufanya kazi hiyo, hujuma. Kwa haraka waliteremka mpaka chini na kukutana na polisi waliokuwa wakiingia katika nyumba hiyo, Madam S kama kawaida yake hakupenda kuingiliana na polisi katika majukumu, moja kwa moja waliparamia pikipiki lao na kwenda mpaka zahanati ya jirani ambako majeruhi alifikishwa kwanza na kutafuta habari kama amekwishakufa au la, daktari wa zamu aliyekuwa bado hajaelewa kinachoendelea aliwaeleza kuwa majeruhi bado hajafa ila ana hali mbaya sana na amemrufaa kwenda hospitali ya Taifa ya Muhimbili.



    §§§§§



    YUJO SUSHI BAR AND IZAKAYA – KAMPALA



    KAMANDA Amata na Zaina (Yaumi) walikuwa wakimalizia chakula cha cha Kijapan ambacho waliamua kwenda katika mgahawa huwo unaomilikiwa na raia wa Japan japo kuonja ladha ya vyakula tofauti kama supu ya Miso na vinginevyo. Walikuwa wameketi kwa muda tu wote wakiwa hawajui nini cha kufanya. Baada ya kamanda Amata kujaribu kupiga simu zote zile ambazo alibuniwa na Chiba na kuzikosa sasa zoezi lilikuwa ni kutafuta namba za mtaa na nyumba ambazo pia zilitokana na namba hiyo.

    “Umefurahia chakula?” Kamanda Amata alimuuliza yaumi.

    “Mmm nimejaribu kula lakini nusu nitapike mh!” yaumi alijibu.

    “Pole, ndio inabidi uonje ladha tofauti sio kila siku wali na maharage tua au ugali na ngege,” Amatab alimtania kisha wote wakacheka na kuinuka tayari kuondoka. Waliletewa bili ya chakula chao, haikuwa gharama, ilikuwa dola za Kimarekani 150 tu, akalipa na kisha akamshika yaumi mkono na kutokanae nje ya mgahawa huo.



    Kwa mwendo wa taratibu walikuwa wakitembea kando kando ya barabara huku Kamanda Amata akiwa kazungusha mkono wake kiunoni mwa Yaumi na Yaumia akafanya vivyo hivyo, hakika walikuwa wapenzi wa ghafla, kila mtu aliwatazama, waliongea na kucheka huku wakisimama hapa na pale. Wakiwa katika mahaba hayo ya dharula kelele za breki za gari zilisikika nyuma yao, Kamanda Amata kwa haraka aligeuka na kumuweka Yaumi nyuma yake, kabla hajakaa sawa, aliona kitu kama jiwe kikimjia usoni, akainama kidogo upande na hapo ndipo aligundua kuwa ilikuwa ni ngumi ya mtu wa miraba mine, hakupoteza nafasi, kwa kitendo hicho Yule mtu alikuwa amemuachia mbavu kamanda zikimchekea, makonde mawili mazito yalifanikiwa kuvunja mbavu moja, hakumpa nafasi akiwa anauguloa maumivu, teke moja kaliu usoni lilimuinua jamaa huyo na kumuweka wima, kamanda Amata aligeuka nyuma hakumuona Yaumi, kachukuliwa.



    “Tulia hivyo hivyo!” ilikuwa sauti ya jamaa mwingine aliyekuwa kamkamata Yaumi na kumkaba akimuweka upande wa mbele yake huku mtutu wa bastola ukiwa umetulia katika shingo ya mwanamke huyo. Kamanda Amata aliuma meno kwa hasira, “Ukivuta hatua moja tu nammaliza huyu mwanamke wako,” Yule bwana alisema wakati alipomuona Kamanda Amata akimjongelea, Amata akasimama, “Weka mikono kichwani,” akaamuriwa, kisha Yule jamaa aliyevunjika mbavu akajikongoja na kumfikia Kamanda pale alipo, pigo moja la uti wa mgongo lilimpeleka chini Kamanda, hakutaka kufika chini mzimamzima alijiwahi na kupiga magoti, Yule bwana akiwa kajishika ubavu wake alizunguka mbela ya kamanda Amata.

    “Ha ha ha ha ha, mchezo umekwisha,” aliongea kwa gadhabu Yule bwana mkono wake bado ukiwa ubavuni. Kutokana na hasira alizokuwa nazo yuloe jamaa baada ya kuvunjwa mbavu moja alivuta teke moja kali ili kumpiga Amata kwa mbele, kosa, kosa kubwa. Kamanda Amata aliudaka mguu na kuuzungusha kwa nguvu zake zote, Yule bwana alipiga yowe kali la maumivu, mifupa ya mguu wake ailiachana, akajibwaga chini, wakatihuo tayari Kamanda Amata alikiwishaichomoa bastola yake na kulenga shabaha makini, alipofyatua alifumua bega la Yule jamaa aliyemshika Yaumi, Yule jamaa akmwachia Yaumi na kuanguka upande wa pili naye akiugulia kwa maumivu. Ile gari ikawashwa na kuanza kugeuzwa, Kamanda Amata hakutaka kuruhusu hilo litokee aligeuka na kuiona ile gari ikiingia barabarani kwa kasi, aliinua bastola yake na kuituliza juu ya mkono wake wa kushoto, alipovuta trigger haikumpa jibu la uongo, ile gari ilipasuka kioo cha nyuma na kuyumba kisha aikagonga nguzo ya taa.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Watu walianza kuja eneo lile, Kamanda Amata akakimbia na kumuinua Yaumi aliyekuwa chini akijaribu kujiinua, akamsika mkono na kuvuka nae barabara kisha akapotelea kenye chochoro za maghorofa yaliyojipanga ng’ambo hiyo ya barabara. Wakajibanza kwenye moja ya kona chochoro hizo wakitazama kinachoendelea.

    “Pole Kamanda,” Yaumi alinong’ona.

    “Pole wewe, mimi haya ndiyo maisha yangu,” Kamanda alijibu, mara simu katika kibanda cha simu ya jamii ikaanza kuita kwa fujo. Kamanda Amata na yaumi wakatazamana. Haikuwa hali ya kawaida kwa simu hizi kuita, mara nyingi hutumika kwa kupiga tu lakini hii ilikuwa inaita bila kukata, Kamanda Amata alishusha pumzi, akachomoa bastola yake na kuifunga kiwambo cha sauti, “Unajua kutumia hii siyo?” alimuuliza Yaumi.

    “”Ndiyo, najua!” yaumi alijibu.

    “Safi, haya shika hii, nilinde naenda kusikiliza simu hiyo,” Kamanda Amata akampa bastola Yaumi kisha yeye akaisogelea ile simu kwa hadhari kubwa. Akaipokea, hakuongea chochote bali aliiweka sikioni tu, aliinua mkono wake wenye simu na kubofya vitufe kadhaa kisha akaiweka karibu kabisa na simu ile.



    “…Tumekwishajua kuwa upo hapa Kampala, na jambo ulilolifanya leo dakika tano zilizopita utalilipa kwa damu yako, hujui unachokitafuta lakini sisi ndiyo tunaojua unachokitafuta na tayari tuko mbioni kukipata kabla yako, hapo ulipo nakuona wewe pamoja na huyo mwanamke uliyenaye, muda wowote naweza kukuangamiza kwa risasi moja tu kama nilivyommaliza mwingine huko Tanzania lisaa limoja lililopita…”



    Kabla Kamanda Amata hajauliza chochote ile simu ikakatika, akaitazama na kuiacha kama ilivyo, hakuirudisha katika kitako chake bali aliiacha ikining’inia. Akatoka na kukiacha kile kibanda akaingia tena pale gizani na kumuta Yaumi yupo makini, akamshika mkono na kuondoka nae akifuata kauchochoro hako kalikokuwa katikati ya maghorofa hayo, akatokea upande wa pili, tax nyingi zilikuwa mahali pale lakini hakuhitaji kukodi hata moja, alitembea kwa hadhari kubwa huku yaumi akiwa pembeni yake.

    “Vipi Kamanda? Nani alipiga simu?” yaumi aliuliza.

    “Simjui, kabla sijamuuliza alikwishakata simu, lakini kasema anatuona na anatufuatilia, nina uhakika na hilo,” Kamanda alijibu. Walitembea mwendo kama wa mita mia tano hivi, nyuma yao Kamanda Amata aligundua kuna mtu anayewafuatilia akija kwa umakini sana akijipitisha kwenye viambaza vya nyumba ili hasionekane nao lakini hakujua kama tayari walimuona. Mbele kidogo kulikuwa watu waliokuwa wakitoka na kuingia katika ukumbi Fulani, Kamanda Amata akamvuta Yaumi na kujichanganya nao huku akimtazama Yule mtu kama anakuja au la, hakumuona, akatazama vizuri hakumuona tena, akapita mpaka mlango wa chooni akaingia na kumuacha Yaumi kaunta, akasubiri kama dakika mbili hakuna mtu, akatoka na kumpa ishara yaumi kisha wakatoke upande wa pili wa jengo hilo na kuingia kwenye tax.



    “Airpot tafadhali,” Amata alimuamuru dereva naye akatii na kuiondoa gari hiyo. Walipoyaacha makazi ya wenye pesa na kuanza kuingia katika viunga vya mji Kamanda Amata alimuamuru dereva asimame, akamlipa ujira wake kisha yeye na yaumi wakaingia mitaani, huku kwetu gtungeita uswazi. Walitafuta nyumba ya kufikia wageni na wakapata moja ya kienyeji zaidi, wakapata chumba, wakajifungia ndani, harufu ya mashuka yaliyokuwa yametumika bila kufuliwa ziliwatesa wawili hao lakini hawakuwa na jinsi.

    “Zaina,” Kamanda aliita kwa upole, baada ya Yaumi kuitika kwa jina lake la bandia Amata aliendelea, “Tupo hatarini sana, inaonekana adui wetu ana mtandao mkubwa sana hadi kujua kama tupo hapa Kampala, naomba nikuulize swali, unakumbuka mara ya mwisho kuja na mumeo Kampala mlifikia wapi au kwa nani?”

    Swali hilo lilimfanya Yaumi atafakari kwa kina, alibaki kimya, kisha akainua uso wake na kumtazama Amata.

    “Kwa kweli nakumbuka tulikuja miaka kama mine nyuma, mume wangu alikuja kumtembelea rafiki yake ambaye ni mfanyabiashara mwenzake, walikuwa marafiki sana hata wakati mwingine walikuwa wakibadilishana biashara zao, sikumbuki nyumbani kwake, lakini ni mfanyabiashara anayejulikana sana, anamiliki mabasi ya abiria ya kwenda nje na ndani ya Uganda,” Yaumi alijaribu kueleza anachokikumbuka.

    “Ok, sasa unakumbuka hiyo kampuni inaitwaje? Nafikiri huyu bwana anweza kuwa funguo wa kile tunachokihitaji,” Kamanda alipata wazo hilo kwa haraka.

    “Yeah kweli Kamanda, sasa sijui kama nitakumbuka lile jina la ile kampuni,” Yaumi alionesha mashaka.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Usijali, hapa haina haja ya kulala, nahisi hatari mbaya katika hili jambo, tuondoke,” kamanda Amata aliamua kuondoka na Yaumi kurudi mjini, moja kwa moja walifika kituo kikuu cha mabasi cha jiji la kampala, mabasi mengi yalikuwa yakiingia na mengine kutoka usiku huo, Kamanda Amata alitulia tuli katika meza ya mama mmoja aliyekuwa akiuza chai na matoke kituoni hapo. Kamanda Amata aliagiza kikombe cha chain a kunywa taratibu huku kaupepo mwanana kakiipendezesha hali ya hewa, ilikuwa tayari saa nne usiku.



    “Kampuni hiyo ilikuwa inaleta mabasi Tanzania?” Kamanda alimuuliza Yaumi.

    “Hapan ilikuwa hailet mabasi Tanzania bali ilikuwa inaunda mabodi yake pale Quality Group kabla hayajaanza kazi, na hiyo yote ilikuwa ikisimamiwa na Kajiba,” Yaumi alijibu. Kamanda Amata alitikisa kichwa chake kuashiria kuelewa jambo.

    “Ok, swali la mwisho kabla hatujaingia kazini, unaweza kukumb uka chochote juu ya briefcase ndogo nyekundu?” Kamanda alihoji.

    Yaumi alijikuta akishtuka kidogo, pale akakumbuka kitu juu ya briefcase ndogo nyekundu, akamtazama Amata usoni, hakuna alichoongea, alionesha dalili zote kuwa kuna jambo amelikumbuka.



    §§§§§



    “Umefanya kazi nzuri sana mwanamke,” sauti nzito ya Matinya ililitekenya sikio la Fasendy, aliyekuwa ameketi kwenye sofa kubwa huku begi lake la mbao lilikuwa pembeni limeegemea ukuta.

    “Haikuwa kazi ngumu kama nilivyotegemea, ilikuwa kama kumsukuma mlevi tu,” Fasendy alijibu huku akiinua glass yake iliyojaa kinywaji.

    “Sawa sasa Yule tayari, bado huyu mwingine wa idara ya Ushuru na forodha, tunachotakiwa ni kupoteza kila anayejua juu ya hili ambaye hayupo kati yetu, yaani tuliyemjuza kwa sababu atufanikishie jambo tu, huyu roho yake naitaka kesho mara tu akikamilisha kusini kabrasha zetu za kutoa mzigo, afe kwa ajali mbaya,” Matinya alisisitiza.

    “Sawa, usiwe na shaka, hizo unazonipa ni kazi ndogo sana kama kumuua mende kwa kumkanyaga mara moja tu.” Fasendy alijibu tena kwa ujeuri.



    Fasendy alikuwa amekutana na bwana Gabriel Matinya jioni ya siku hiyo katika nyumba yake ya falagha iliyopon huko Temeke, akimpongeza baada ya kazi tamu ya kuondoa roho ya Jaji Ramson kwa kumdungua jioni ya siku hiyo nyumbani kwake mara tu alipokuwa amerejea kutoka kazini na kuketi kwa chai ya jioni mezani kwake. Hakufanya makosa, alitekeleza lile alilotumwa, na bunduki yake anayoipenda sana katika kazi hiyo ya udunguaji AK 47, sasa anabadilishiwa zoezi, anatakiwa kumuua bwana Gomegwa, meneja wa idara ya ushuru na forodha mara tu amalizapo kusaini kabrash a za kutoa kontena lao pale bandarini.

    “Fasendy, kuna mtu mmoja amekwishaingia katika mchezo huu na huyu mtu ni hatari sana, hatari kuliko hatari yenyewe.”…..





    “Nani huyo hatari kuliko hatari yenyewe? Nimepambana na hatari kuliko hiyo unayoizungumzia, nina uwezo wa kumdhibiti kama ninavyomdhibiti chawa kwa kidole change,” Fasendy alitamba.

    “Mh! Fasendy, huyo jamaa ni hatari, Tanzania inamtegemea sana kwa kazi ngumu za hatari na utata, na hakuna kazi aliyoshindwa mpaka akaitwa TSA yaani Tanzania Secret Agency namba 1, na sasa tayari yuko Kampala kwa sakata hili, sikutaka kabisa huyu bwana aingie katika hili lakini sijui siri imevuja wapi…!” Matinya alionekana wazi kuchanganyikiwa.

    “Ok, nimekuelewa, sidhani kama huyu meneja wa Idara ana madhara sana, unaweza kutuma vijana wako wakammaliza, mimi nikamfungie kazi huyo wa Kampala,” Fasendy alitoa wazo.

    “Uko sahihi, kule Kampala tayari tulishaweka watu sawa kumshughulikia lakini taarifa zilizonijia hivi punde ni kuiwa kawatoroka na kawaachia majeraha makubwa, mmoja keshauawa, sasa hapo ujue kitaalamu huyu jamaa keshakuwa mbogo na hatujui kajificha wapi, je ni haraka gani waweza kuitumia kufika Kampala kabla ya alfajiri?” Matinya aliongea kwa wasiwasi.



    “Usijali, mimi ndio Fasendy, Comando wa kike, Somali Land wenyewe wanajua nkazi yangu, Al shabab wenyewe hapa wanakaa chini, naweza kukuhakikishi nitakuwa Kampala kabla ya saa kumi alfajiri na kazi ya kummaliza huyo bwege itanichukua lisaa limoja tu pindi nikanyagapo ardhi ya Museven,” Fasendy aliongea huku akijipigapiga kifuani kuonesha ugangwe.

    Fasendy na Matinya waligonga cheers na Fasendy akajimiminia kinywaji chote kisha akainua kibegi chake ambacho ndani yake kuna Yule mwana mkiwa AK 47 na vikorokoro vingine.

    “Count on me!” Fasendy alimwambia Matinya kisha akaiacha ile nyumba na kupotelea kusikojulikana.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    ‘Kama kuna mtu ananipa matumaini kwa sasa ni Fasendy,’ Matinya alijiwazia kisha akajiinua na kuingia chumbani alikomuacha Marina akikoroma.



    §§§§§



    Madam S na Chiba walisimama bila kuwa na neno lolote, wakiwatazama wauguzi wa chumba cha wagonjwa mahututi wakilivuta shuka jeupe na kuufunika mwili wa Jaji Ramson ambaye alikata roho dakika chache tu zilizopita, hakuongea kitu chochote na Madam S zaidi ya kumtazama kwa macho yake maangavu. Haikuwa kawaida kwa Madam S kuangusha chozi lakini hapa alijikuta tayari chozi lake limefika sakafuni, Jaji Ramson hakuwepo tena, Jaji kijana aliymhukumu Yaumi kunyongwa takribani wiki tatu tu zilizopita. Chiba alimvuta pembeni Madam S na taratibu akatoka nae nje.

    “Madam, unafikiri hili linahusiana na kisa cha Yaumi?” Chiba aliuliza.

    “Asilimia mia, nina uhakika, toa hiyo simu kwanza iwashe tuangalie kilichopo,” Madam S alimwambia Chiba. Wakiwa wameketi katika moja ya vibanda vya kupumzikia Chiba aliiwasha ile simu na kuperuzi mawili matatu, meseji moja tu ilikuwa inbox, akampa Madam S aisome.



    ‘…kwa nini tubishane wakati kazi ulishaimaliza? Hundi tuliyokupa inatosha kwa kazi uliyofanya, na ukileta kujua utajutia uamuzi wako…’



    “Kwa vyovyote kazi hiyo ni ya kumhukumu Yaumi, umeona sasa?” madam S alimwambia Chiba.

    “Sasa Madam, tuitafute hiyo hundi tuziunganishe na zingine tufananishe mwandiko na saini iliyopo tuone kama vinaona maana zile mbili za Chilungu zimefanana, sasa tuone nah ii nayo ikiwa sawa na zile, tayari hatuna la kuuliza,” Chiba alitoa wazo, wote wakasimama na kuondoka eneo hilo.

    Chiba alimuacha Madam S nyumbani kwake kisha yeye kuendelea na kazi ya kuitafuta hiyo hundi, alirudi nyumbani kwa marehemu usiku huohuo.



    TUREJEE KAMPALA



    “Nakumbuka baada ya marehemu mume wangu kurudi na ile briefcase nyekundu nyumbani na mimi kushindwa kuifungua, aliivinja kisha akatahayari sana na kile alichokiona ndani ya briefcase hiyo, usiku huo alikesha akisoma makaratasi mengi yaliyobanwa pamoja, na asubuhi nilimuona akiwa hana raha kama awali, alitoka na kununua briefcase nyingine kama ile ile akaweka baadhi ya nyaraka hizo, akanituma niende benki kuituma, sasa nakumbuka ile briefcase niliituma kwenda Uganda, kwa huyo rafiki yake, nakumbuka sana, sikumbuki ile anwani lakini nakumbuka nilituma hiyo briefcase,” yaumi alieleza kwa kirefu.

    “Safi sana, sasa unaweza kukumbuka lini uliipeleka hiyo briefcase posta na ni posta gani pale Dar es salaam?” kamanda Amata aliuliza, wakati huo tayari walikuwa wameliacha lile benchi la chain a kujivuta pembeni kuliko na vurugu nyingi za vijana wanaogombania mizigo ya wasafiri usiku huo.



    “Nakumbuka, ilikuwa ni miezi mitatu ilopita, nilitumia ofisi ya posta mpya pale Azikiwe, kama unakumbuka siku ile kulipokuwa na maandamano ya vyama vya upinzani na kusababisha ile barabara kufungwa,” yaumi alijibu.

    “Ok nakumbuka tarehe, sawa, sasa saa moja inatutosha kujua ni wapi ulituma mzigo,” Kamanda Amata alimwambia Yaumi, lakini alimshauri kutafuta mahala salama kujificha japo kwa dakika sitini tu ambazo watakuwa wanasubiri jibu. Kamanda Amata alimpigia simu Gina ili awasiliane na mkuu wa posta usiku huo na ikiwezekane apate taarifa juu ya mzigo huo usiku huohuo.

    Yaumi akiwa na Amata waliachana kila mmoja akichukua njia yake ili kuwapoteza kama kuna wanaowafuatilia. Katika kituo hicho cha mabasi kulikuwa na nyumba nyingi za kulala wageni, Yaumi alichagua mojawapo na kwenda kuchukua chumba, kisha Kamanda Amata akafuata, akiwa anatembea kwa tahadhari kubwa sana, aliiendea ile nyumba ya wageni na kuingia kisha akaketi katika viti vya mapokezi, hakuingia chumbani, aliketi mahala hapo akitazama televisheni kubwa iliyofungwa hapo mapokezi, wafanyakazi hawakuwa na tatizo walimuacha apumzike. Mkononi mwake alikuwa ameshika jacket la ngozi ambalo lilifunika bastola iliyoshikwa kwa mkono wa kuume. Kwa ujumla walijipanga, Yaumi alikuwa na bastola nyingine kutoka kwa Kamanda Amata, akiwa anafuata maelekezo sahihi anayopewa na Kamanda huyo.

    Yaumi aliingia chumbani na kutulia tuli bila kuwasha taa yoyote mle ndani, aliketi kitandani na bastola mkononi tayari kwa lolote, alishukuru sana kwa kupitia mafunzo ya JKT mara alipomaliza shule miaka mingi nyuma, na sasa anaona mafunzo hayo yanavyomsaidia, alitazama kidubwasha alichopewa na Amata na kuambiwa kikipiga alam tu, ajue kuwa Kamanda matatani.



    Saa moja ilitosha kwa Gina kukamilisha kazi hiyo kama alivyoamuriwa na bosi wake, alipata tafutishi zote alizoagizwa juu ya ule mzigo, tarehe uliotumwa, kwa nani, alinakiri kila kilichotakiwa na alipohakikisha kuwa amekamilisha alitoka katika ofisi hizo usiku huo wa saa tano ikiwa ni karibu na saa sita, moja kwa moja akaingia katika gari yake na kuketi nyuma ya usukani, jambo la kwanza kabla ya yote alituma kwa njia ya meseji ujumbe ulea na kuufuta katika simu yake na kishapo akachana ile karatasi katika vipande vidogovidogo na kuimwaga kwa nje, akawasha gari na kugeuza, akaingiza barabarani kama anaelekea posta ya zamani kwa mwendo wa wastani.



    Palepale alipoketi Kamanda Amata alijikuta ameketi na mtu mwingine aliyevalia pama kubwa na fulana nyeusi, hakuonesha dalili yoyote ya kuwa na ubaya na Amata, mara simu ya Kamanda ikaita kuashiria kuna ujumbe umeingia muda huo, akaingiza mkono wa kushoto mfukoni kuitoa ile simu.

    “Nilikuwa naisubiri hiyohiyo!” sauti ya Yule mtu ikamfikia Kamanda Amata, wakatazamana, kwa kuwa pale mapokezi palikuwa na watu mbalimbali wawili hawa hawakutaka kuonesha uadui. Kamanda Amata aliendelea kumkazia macho kijana huyo aliyejiamini, “Lete simu!” aliendelea kumuamuru Amata huku akimsukasuka kwa mkono wake.

    “Unataka nini kwenye simu yangu?” Amata akauliza.

    “Mi nataka simu, sikutaki wewe,” Yule jamaa bado alikuwa akimhimiza Kamanda. Mara mlango wa kuingia vyumbani ukafunguka, Yaumi akatokea alipotazamana tu na Kamanda alielewa kuwa tayari Kamanda wake yuko katika mtihani, Yaumi aliketi katika viti vinavyotazamana na na vile vya upande alioketi Kamanda Amata, wakawa wakitazamana, Kamanda Amata akampa ishara ya macho Yaumi kuwa atangulie nje, nae akafanya hivyo, haikuchukua muda Yule bwana aliyekuwa aking’ang’ania simu alitulia tuli, Kamanda Amata akamuegemeza vizuri katika kile kiti, bastola ya Kamanda iliyokuwa imefutikwa ndani ya koti lake, kisha yeye akainuka na kutoka mpaka nje, akamshika mkono Yaumi na kupotelea gizani.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wakiwa katika moja ya vichochoro vya eneo hilo, aliichukua simu yake na kuusoma ujumbe ule,





    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog