Search This Blog

Sunday 22 May 2022

RISASI NNE - 3

 







    Simulizi : Risasi Nne

    Sehemu Ya Tatu (3)





    Siku ilofuata, Joru alikuwa akitembea tembea kuangalia mandali ya shamba la Shibagenda lililojaa Migomba iliyozaa vizuri na mazao mengine, akifuatana na watoto wa Shibagenda walioonekana kumpenda sana. Nyumba hiyo haikujengwa mbali na kambi ya Mtukula, na wala haikuwa mbali sana na mpaka wa Uganda na Tanzania, Joru alijua Shibagenda kamsogeza karibu na azma yake. Alihakikisha anaishi kwa amani na familia hiyo, akiwatumikia kwa upendo mkubwa, akfanya kazi mbalimbali za shambani bila kinyongo, alijua kupanga ratiba zake za kazi hivyo aliweza kupata nafasi ya kutembea hapa na pale akitazama hili na lile.

    Ni miaka mingi sana ilikuwa imepita tangu Joru aondoke Mtukula baada ya vifo vya wazazi wake na kuteketezwa kijiji chake, ilikuwa ni zaidi ya miaka 15. Siku hii Joru alikuwa amekwenda sokoni kununua hiki na kile. Maisha kwa ujumla yalikuwa ya fuaraha hayakuwa yale ya hekaheka tena, yale ya kulala juu ya miti tena, hapana, haya yalikuwa ya utulivu, yalikuwa yale ya kulala kwenye kitanda safi, ya kula chakula safi, Joru alianza kubadilika, alianza kunawili, kwa kuwa sasa alikuwa ametulia, Joru alikuwa akifanya mazoezi kila siku asubuhi na jioni, ya kukimbia, kunyanyua vitu vizito, baada ya Muda Joru akawa katika hali nzuri, akawa na siha bomba ya kiume, kila aliyemuona alimhofia. Joru aliunga na kikundi cha Karate kilichopo maeneo ya Mtukula sokoni, Shibagenda na mkewe hawakuwa na kinyongo na hilo.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Mwaka ulipita Joru alikuwa na uwezo wa kujilinda kimapambano, ijapokuwa hakuwa na renki yoyote katika mchezo huo lakini alijikuta anaweza japo kupambana na kibaka na kumdhibiti kwa makofi kadhaa. Kutokana na familia hii kumpenda sana Joru, hawakutaka kabisa kijana huyu aondoke hapo, kila alipoaga kuwa atarudi baada ya siku tatu, ilikuwa ngumu kumuachia na wakati mwingine walikuwa wakimuachia kwa shingo upande tu.

    Mwishoni mwa juma Shibagenda alikuwa akija kupumzika shambani kwake, siku hiyo alikuja na kukutana na Joru wakawa katika mazungumzo ya hapa na pale.

    “Sasa kaka, mi naona muda umefika, uniruhusu nikatafute maisha mahali pengine,” Joru alimwambia Shibagenda.

    “Yah, naelewa unachosema Joru, ni kweli sasa unastahili hata kuwa na mke, lakini Joru, unaonaje ukisubiri japo mwaka mmoja tu ili nipate mtu wa kukaa hapa nawe nikuruhusu,” Shibagenda alimwamba Joru, Joru hakukataa. Mara nyingi aliombwa hivyo nye hakuwa na kinyongo kwa maana hakuwa na shida ya pesa, kama pesa alikuwa akipewa nyingi na Shibagenda, mpaka hapo alikuwa na kitabu katika benki ya posta, hivyo haikuwa tatizo. Akaendelea kuishi hapo na kuendelea na shughuli zake kama kawaida.



    “….Maisha ni uvumilivu, mvumilivu hula mbivu, usilazimishe tunda kuiva, subiri wakati wake, likiiva litaanguka lenyewe, siku yako inakuja ….”



    Ilikuwa ni kama sauti ya mtu iliyokuwa ikipita masikioni mwa Joru alipokuwa amesinzia katika kibaraza cha nyumba anayoishi.



    §§§§§



    6 rejea MTUKULA JESHINI



    HILI ni jambo ambalo Joru hakulitegemea hata kidogo, alibaki mdomo wazi hakujua ni nini kinatukia mbele yake, kama ilivyo ada kuwa kila aliyepata zawadi alilakiwa na ndugu zake na kupewa zawadi mbalimbali, Joru alijua kuwa akipokea zawadi hakutakuwa na yeyote kwake wa kumpa zawadi. Alipopokea zawadi ya vyeti vyake vilivyomstahili, machozi yalikuwa dhahiri, shahiri katika macho yake, Shibagenda alilielewa hilo alipokuwa akimtazama Joru na kumkabidhi mgeni rasmi vyeti hivyo vinavyomstahili kijana huyo, Joru alivipokea, akapeana mkono na wakuu hao, akarudi nyuma hatua moja akapiga mguu chini na kutoa saluti kisha akageuka kwa ukakamavu alipokuwa akitoka eneo lile kurudi katika mstari wake, alimuona mke wa Shibagenda na watoto wake wawili wakija kasi huku wakipiga vigelegele. Joru alitabasamu na kuifungua mikono yake akawakumbatia watu hao waliopendana sana, huko nje kila mtu alikuwa akishangilia Joru! Joru! Joru! Joru!...



    “…Usiseme kuwa katika dunia hii hauna ndugu, ndugu ni wale wote uliowatendea mema, tenda mema uende zako usingoje shukrani, kesho utaona makandokando yake…”



    Joru alikuwa akijiwazia moyoni, akiikumbatia familia hiyo kwa furaha, akiwanyanyua wale watoto wa Shibagenda kwa furaha, miruzi ilitwala uwanja mzima.



    Walipokuwa wakitoka pale uwanjani, Joru alimuona binti mmoja aliyekuwa akipenyapenya kwa shida kwenye kundi la watu, Joru akamtazama, sura haikuwa ngeni sana. Binti Yule alikuwa na motto katika bega lake, alipopata nafasi akatembea kwa mwendo wa haraka kumuwahi Joru kabla hajafika katika mstari wake, Joru akasimama akimtazama, Joru akavuta hatua kumuwendea msichana huyo, vifijo na nderemo viliongezeka uwanjani. Yule binti akamkumbatia Joru kwa nguvu huku akilia machozi, Joru alimbembeleza, akamtazama Yule motto pale begani, Yule mtoto akacheka, alikuwa na meno manne tu kinywani mwake.

    “Hii ndiyo zawadi yako, huyu ni mtoto wako….” Yule binti akamwambia Joru, Joru alimtazama kwa tuo.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Nione mara baada ya shughuli hii,” akamjibu kisha akawaacha na kurudi kwenye ule mstari. Baada ya tukio hilo sherehe ile ilifikia tamati awamu ya kwanza, sasa ilibaki ni burudani na mazungumzo na marafiki, ndugu na jamaa.



    Watu wote walimwagika uwanjani wakiserebuka na muziki mzito uloiokuwa ukipigwa katka eneo lililoandaliwa, kama unavyojua, ndugui, wazazi na marafiki walikuwa mekuja na mpochopocho mbalimbali ili kushereheka na wahitimu wao, ndugu zao, watoto wao.

    “Hongera sana Joru!” mke wa Shibagenda alimpongeza huku wakipeana mikono, na watoto wake wakafanya vivyo hivyo. Joru alikuwa na furaha sana kwa kumaliza mafunzo yake. Akiwa katika mazungumzo hayo mara askari mmoja akamfuata.

    “Joru, unaitwa ofisini,” aliambiwa. Joru alishtushwa na wito huo, akaagana na mama Shibagenda na kuelekea alikoitwa.

    Kilikuwa chumba nadhifu chenye samani za bei mbaya, lakini zilizochongwa na vijana wa jeshi wenyewe. Alikaribishwa na binti mmoja aliyevalia nadhifu kabisa, Joru akapita ndani na moja kwa moja akakutana na brigedia Shibagenda.

    “Karibu kiti Joru, karibu sana,” Joru alikaribishwa na Shibagenda, akaketi kiti kinachotazamana mara tu baada ya kupeana mikono. Kabla Shibagenda hajaongea lolote, Joru akaanza na yake.

    “Kwanza samahni sana mkuu, nilitoka nyumbani bila kuaga na kujiunga na jeshi katika mazingira ya kutatanisha, wakati wewe ulipoondoka nilipata fununu za ajira jeshini, nikajua wazi nikimuaga mama naye atakushirikisha wewe hivyo nilikuwa nafanya utaratibu mwenyewe kimyakimya…



    >>>>>rejea Mtukula kwa Shibagenda<<<<<<



    JORU akiwa bado anaishi kwa Shibagenda, alipata tetesi za ajira za vijana kujiunga na jeshi, alijaribu kuzifuatilia bila ya kumshirikisha mtu. Kwake haikuwa tabu sana kwani wakati huo bosi wake Shibagenda alikuwa amesafiri kikazi kwenda nchi ya ng’ambo kwa miezi miwili, Joru alifanikiwa zoezi la kujiandikisha jina lake. Lakini wakati wa kukaguliwa vyeti vya shule, Joru hakupata nafasi kwa kuwa elimu yake ilikuwa ni ya shule ya msingi tena darasa la nne ila tu alijua kusoma na kuandika vyema. Joru alisikitika sana kuikosa nafasi hiyo, lakini moyoni mwake hakukubali kushindwa.

    “Sasa wewe hauna hata cheti kimoja, hapa umekuja kufanya nini?” mmoja wa wakaguzi alisema.

    “Samahani afande, sikujua kama jeshio linahitaji watu waliosoma, mi nilidhani upiganaji na ufyatuaji risasi ni uwezo wa mtu yeyote, lakini sina uhakika kama vyeti vinaweza kuonesha umahiri wa mtu kuilinda nchi yake,” Joru alijibu.

    Yule mkaguzi aliyekuwa na cheo cha luteni usu alikasirishwa na majibu hayo, akamwita MP amkamate Joru na kumpa adhabu kali. Ilikuwa ni siku mbaya kwa Joru, alaitumbukizwa kwenye bwawa la maji machafu na kuambiwa aogelee kwa kupiga mbizi na kuibuka, baada ya adhabu hiyo iliyochukua takribani dakika thelathini, Joru akiwa ametota kwa tope na uchafu aliambiwa akimbie uwanja wa gwaride huku akipigwa bakora za nguvu. Kisha akaamuriwa kulala chini, chali wakati wa jua kali mpaka wenzake watakaporuhusiwa kuondoka, baada ya zoezi lote kukamilika Joru alitakiwa kuondoka eneo lile na asirudi tena. Joru akaondoka kwa unyonge kurudi nyumbani, alifika na kulala, mama Shibagenda alimletea chakula na kumuuliza kilichomsibu, Joru hakumwambia kitu alijifanya tu anaumwa.



    Baada ya wiki moja, wale wote waliotakiwa kurudi, walikuwa kama vijana hamsini hivi, walifika tena pale kikosini kwa ajili ya awamu nyingine ya usahili. Siku hiyo jopo la wakaguzi liliongezeka, alikuwepo msaidizi wa mkuu wa jeshi mkoa wa Kagera, daktari wa jeshi mkoa Dr Janeth Ishengoma alikuwapo kwa ajili ya kuhakikisha afya za walengwa hazina mgogoro. Wakiwa tayari katika mstari maalum nje ya hema lililoandaliwa tayari kwa ajili ya kazi hiyo, Joru aliibukan tena siku hiyo, Joru hakukubali kushindwa katika zoezi hilo alidhamilia tangu moyoni, ‘kama kuniua waniue tu’, alikwenda mpaka pale lakini hakujipanga kwenye ule mstari, alisimama mbali kidogo.

    Ilikuwa siku ya vipimo vya afya, MP mmoja alipita eneo lile na kumuona Joru kasimama pembeni akiwa kavalia fulana yake nyeusi na jeans ya bluu ‘LEE’

    “Wewe,” akaita Yule MP, akamtazama Joru juu mapaka chini, “Mbona umekaa mbali na wenzako, hutaki jeshi ee?” akauliza kwa ukali, Joru akasimama akimkazia macho, “Nakuuliza hutaki jeshi?” Joru aliona swali hili linalorudiwa mara mbili lina maana sana kwake.

    “Nataka afande,” akajibu.

    “Haya kwenda kwa wenzako pale, simama mstari ala!” Yule MP aling’aka. Joru akajiunga katika mstari akawa nafasi ya mwisho. Moyoni mwake aliwaza, waliochaguliwa ni mia moja vipi wakikata mstari mpaka mtu wa mia moja nay eye ni wa miamoja na moja? hakupata jibu, ‘liwalo na liwe’ akajipa moyo na kupiga moyo konde. Mstari ule ukazidi kwenda, alipata moyo pale alipoona siku hiyo hakuna maswali ya vyeti wala elimu wala kuitwa majina. Joru alisimama mbele ya meza yenye vifaa tiba lukuki kwa ajili ya zoezi hilo.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Kaa kitini,” muuguzi aliyekuwepo alimwambia Joru, naye akaketi akiwa ana hofu yasije kutokea yale ya wiki iliyopita, “Tulia mwanaume, mbona una hofu sana, au hujiamini?” Yule muuguzi akamuuliza. Akampima Joru kifua na presha akaandika kwenye kijitabu chake, kisha akachukua sindano na kumtoa damu kwenye mshipa akaibandika kikadi Fulani kisha akamwuliza jina, akalizndika kwenye kile kijikadi na kitabu chake, akamruhusu aende kwa wengine. Hatua ya upimaji ikakamilika. Baada ya hapo wakaja MP wane wakawachukua wale vijana na kuwagawanya makundi manne ya watu ishirini na tano kila moja, mchakamchaka ukaanza. Walitakiwa kukimbia mchakamchaka wa kilomita sita kwenda na sita kurudi bila kupumzika. Zoezi hilo kw Joru lilikuwa kama kumpiga chura teke. Nyuma wakifuatwa na gari moja ya jeshi, maalumu kwa kubeba wote watakaozimia njiani. Wakiwa njiani kwenda huku wakiimba nyimbo, vijana wengi walionesha udhaifu na kuanguka ovyo wengine wakilalamika vichomi, mmoja wa vijana hao aliyekuwa akikimbia sambaba na Joru alianza kujishika mbavu na mara akapunguza mwendo akaanguka chini akiwa hana uwezo hata wa kupumua, MP akaamuru Joru na mwingine wambebe kumpeleka garini huku wenzao wakiendelea na mchakamchaka. Walipofika kwenye ile gari na kufunguwa mlango walimpakia kijana huyo ndani kulikuwa na wengine wawili. Joru wakati anatoka, alipita karibu na dirisha la mbele upande wa kushoto wa gari hilo. Dr Janeth Ishengoma alimuona Joru, akashtuka kidogo, ‘Huyu sio Joru?’ akajiuliza lakini akatulia akiendelea kumwangalia kijana huyu aliyekuwa akikimbia huku akiimba kila wimbo unaoanzishwa na MP hao.



    §§§§§



    Vijana kumi na mbili walionekana kushindwa kabisa, walirudishwa na kufikia hoapitali ya jeshi hapohapo Mtukula. Mistari mine iliyo sawa ikapangwa mbele ya lile hema la kupimia afya kwa ajili ya matangazo machache. Mara hii Joru alimuona Dr Janeth katika ya wale wanajeshi waliokuwa wakiongea pale mbele, alijisikia vibaya kidogo kwa kuwa alikumbuka alipotoroka nyumbani kwa daktari huyo. Baada ya matangazo hayo ya kutakiwa kurudi baada ya siku saba tena kwa ajili ya majibu ya afya na kujua nani kachaguliwa na nani la, Yule mkuu wa jeshi msaidizi alimwita tena Joru mbele yake, akiwa na waambata wengine wa jeshi.

    “Hivi wewe kijana, siku ile si nilikufukuza, sasa leo umekuja kufanya nini?” aliuliza.

    “Nimekuja jeshini afande,” Joru alijibu bila kuogopa maana alikwishajua kitakachofuata. Yule mkuu akawaeleza wale wengine alichomfanya kijana huyo wiki moja iliyopita na leo karudi tena. Dr Janeth alisikitika sana kwa adhabu aliyoisikia kuwa Joru alipewa na MP siku hiyo.

    “Mtazame huyu kijana mkuu, ana umbo la mazoezi, amejengeka vyema, umempa adhabu na leo kaja tena, unaonaje kama huyu akiwa mwanajeshi wako jasiri atayekuwa mstari wa mbele katika mapambano na adui, ana kiu na nchi yake labda ndio maana karudi tena, anahitaji, mpe nafasi akashindwe mwenyewe,” Dr Janeth alizungumza. Joru alifarijika kwa maneno hayo.

    “Una wazazi wewe?” Yule mkuu aliuliza, lakini alichokishuhudia ni uso wa Joru uliobadilika ghafla.



    “Sina wazazi,” akajibu.

    “Sawa, kaa pale juani nitakuita, inaonekana una kichaa wewe, sio bure,” Yule mkuu akamwambia Joru kisha akaondoka na jopo lake. Dr. Janeth alimtazama Joru kwa huruma akiwa anaketi pale juani kisha akageuka na kuondoka kurudi hemani, akapekua vipimo vyote na kupata vile vya Joru, akacheki majibu yake ya awali alikuwa amzima wa afya, hii ilimpa faraja kidogo lakini kwa kuwa alijua kuwa kijana huyu hakufaulu upande wa elimu, na alijua wazi utata wa mkuu wake hivyo alishikwa na hofu juu ya hatima ya Joru.

    Siku hiyo Joru alipewa adhabu nyingine ya kuchimba mashimo ya takataka katika nyumba za jeshi, mashimo mawili makubwa, Joru aliifanya kazi hiyo na kuimaliza saa kumi nambili jioni akiwa hoi kwelikweli. Joru aliendelea kuvumilia yote moyoni akiwa na moja tu kuingia jeshini. Baada ya kumaliza aliruhusiwa kuondoka na hakuambiwa kitu chochote na afande aliyekuwa akimsimamia. Joru alitafakari hatima yake hakujua ni nini kinaendele, aliamua kutokata tama. Alirudi nyumbani akiwa hoi, akaoga na kulala, siku iliyofuata akaendelea na kazi zake kama kawaida za hapo nyumbani kwa Shibagenda.



    Baada ya wiki moja, ilifika siku ya kwenda tena jeshini, Joru hakujali kitu aliaga kwa mama Shibagenda lakini hakumwambia anakwenda wapi. Alifika pale na kuwakuta vijana wengine wameshafika. Baada ya mudamfupi ikapigwa filimbi na wote wakatakiwa kujipanga, mara akaja Yule mkuu wa jeshi msaidizi na waambata wengine wawili, siku hiyo Dr. Janeth hakuwepo, wakaanza kuita majina ya wote waliofaulu, vijana sabini na sita walipata nafasi, lakini katika majina yote hayo jina la Joseph Rutashobya halikuwapo. Joru aliumia sana na hali hiyo, alimtazama Yule mkuu wa jeshi kwa jicho bay asana lakini afanyeje, wakatakiwa kuondoka lakini wale waliofaulu wakatakiwa kuripoti siku ya tatu ili kambi ianze rasmi. Joru akaondoka, hakutaka kuongea na yeyote jambo lolote.

    Siku ya tatu,Joru alikuja, mkononi akawa na mfuko mdogo wa Rambo wenye surari moja ya jeans na fulana moja pamoja na vitu vidogodogo vya usafi wa mwili wake, alifika na kubaki nje ya geti kwa muda akiangalia mazingira, baada ya muda kidogo aliingia getini na kuripoti katika kibanda alichokuwa ameketi mlinzi, akaambiwa akae chini asubiri wengine. Ndani ya masaa mawili vijana wote walikuwa wmefika, ilikuwa tayari saa kumi jioni, jina la mmoja mmoja likaanza kuitwa, kama kawaida Joru hakuwapo kwenye orodha, Yule mlinzi akamwita.

    “We mbona jina lako halipo?” akauliza Yule MP

    “Sijui kwa nini, lakini mpaka jana lilikuwepo,” Joru akajibu kwa kujiamini. Wale MP wakaongea paembeni kisha mmoja akachukua ile orodha na kuondoka nayo na kuwaacha vijana kwa Yule Mp mmoja.



    “Haya panga mistari mitatu hapa, weka na mzigo wako kichwani” Mp akatoa amri, vijana wakajibanga, kila mmoa alikuwa na mzigo wa ukubwa wake, walitakiwa kujitwisha kichwani, kama una sanduku haya, kama ni box haya. Joru pekee alikuwa na kijimfuko hicho cha plastiki akajitwisha kichwani, wakaanza kukimbizwa jogging, Mp akipiga filimbi mnakwenda mbele akipiga tena mnageuka na kurudi na mizigo yenu kichwani. Lilikuwa ni zoezi gumu la masaa mawili, baadae waliongozwa mpaka mbele ya ofisi moja iliyotengenezwa kwa mabati, wakapangwa pale mbele mistari mitatu kila mmoja akiwa bado na furushi lake kichwani, majina yakaanza kuitwa, likiitwa askari mwingine anasikiliza sauti ilipotokea anakurushia buti mpya, chombo cha chakula ‘Mess tin’, unatakiwa uvidake bila kuangusha mzigo wako kichwani, ukiangusha tu adhabu kali. Watu wakaitwa, lakini hakuna aliyefaulu kudaka bila kuangusha wote wakaangusha mizigo yao na kusubiri adhabu. Joru hakuamini aliposikia jina lake likiitwa la mwisho, alitabasamu kiasi kwamba aliona kama mbiongu zimefunguka, zikarushwa buti akazidaka kwa kidole kwa kuinasa kamba iliyoziunganisha huku mkono huohuo akikamata mess tin iliyofika sekunde chache tu nyuma ya buti hizo, mzigo wake haukuanguka. CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Safi sana, Joseph,” alitamka Mp mmoja kisha akawageukia wale wengine, “Hivi ninyi mnafikiri mnakuja nhapa pikniki, mabegi makubwa ya nini, hakuna fashion show hapa, angalieni mwenzenu, huyu ndiye mwanajeshi wa kweli, anajua analofanya, tazameni alivyodaka hivyo vitu hakuna kilichomuanguka, sasa yeye ataendelea na utaratibu mwingine na nyie kwanza mnakwenda pond kuongea na watoto wqa kambale, haya weka vitu vyenu hapo chini,” akawaamrisha, wakavibwaga na wote kupelekwa kwenye adhabu ya kuoga matope. Joru alichukuliwa mpaka kwenye ofisi ya msajili, akasajiliwa kwa mara ya mwisho kisha akapewqa, nguo zake za mafunzo, begi la kijeshi, kofia ya chuma na vitu vingine akaoneshwa bweni, akaenda na kujichagulia kitanda cha kona.

    Joru alianza mafunzo makali ya jeshi na vijana wengine kwa muda wa miezi tisa katika mvua na jua, vumbi na umande, alionesha umahiri mkubwa katika kila Nyanja, kutumia silaha, shabaha, Joru alionesha umahiri mkubwa katika kulenga shabaha, mpaka anamaliza kozi ile hakuwahi kukosa hata risasi moja, katika michezo ya mapigano, Joru alikuwa tayari ana uwezo mkubwa tangu mitaani hivyo ilimchukua muda mfupi tu kuweza kuwa juu ya wengine katika hilo, alikuwa akicheza karate na kungfu kama mtu aliyepatwa kichaa.



    >>>>>>…rejea Mtukula Jeshini<<<<<<<



    “Joru, umenidhihirishia msemo wa wahenga, atafutaye hachoki na akichoka keshapata,” Shibagenda alimwambia Joru huku akimpa mkono, “Hongera kwa kuhitimu mafunzo, nimeona umahiri wako wa hali ya juu, nimesikia sifa zako mara tu nilipofika ijapokuwa sikujua ni Joseph gani lakini leo ndiyo nimejua kuwa ni wewe, wewe ni jasiri, mwanaume anatakiwa kuwa hivyo kama ulivyo wewe, nilimwambia mke wangu wiki moja iliyopita kuwa upo jeshini alishangaa sana kwa sababu niliporudi waliniambia umetoroka nyumbani hukuaga, niliumia sana lakini sikuwa na la kufanya,” Shibagenda aliongezea.

    “Asante Mkuu, nilijua wazi usingeniruhusu kuja jeshini ndio maana sikuaga mtu, samahani kwa hilo,” Joru aliomba msamaha.

    “Usijali Joru, wewe ni mwanangu, nakujua kuliko wote hawa, sasa ile nyumba pale nyumbani ipo kwa ajili yako, muda wowote, ukitaka kuja uje pale, upumzike pale, hata kama utataka kuoa basi muweke mke pale wakati wewe uko kambini kwa sababu sheria unazijua, sivyo?” Shibagenda akaendelea kuzungumza na Joru.

    “Ndiyo mkuu, asante kwa moyo wako wa pekee,” Joru alishukuru, akasimama na kupiga saluti kisha akatoka nje na kuwakuta watu wakiendelea na sherehe, alipokuwa akitoka tu mlangoni akakutana na Dr. Janeth Ishengoma.



    “Hongera sana Joru, nimeona kazi, hakika jeshi lilikuwa linahitaji mtu kama wewe, sina muda wa kukaa hapa, nafikiri unanikumbuka, na unakumbuka ninapoishi, Biharamulo kikosi namba KJ 756Y, naoma uje, naenda kuandaa zawadi yako nzuri sana, utaikuta pale, niambie utakuja lini?” Dr Janeth alimpongeza na kuomba miadi.

    “Dr, kwa kuwa kuanzia kesho tutakuwa na mapumziko ya wiki mbili kabla ya kupangiwa kazi na kikosi cha kwenda, nitakuja mwisho wa juma hili,” alijibu.

    “Karibu sana,” Dr janeth akamalizia na kumbania jicho kisha akaingia kwenye jeep ya jeshi tayari kwa safari. Joru akaja kuungana na familia ya Shibagenda kwa chakula cha mchana kilichoandaliwa na familia hiyo. Joru akawa kama ameshtuka hivi, akaacha kwanza kula.

    “Joru vipi?” aliuliza mke wa Shibagenda.

    “Subiri, kuna kitu nimekumbuka, akainuka na kuondoka,”





    Joru alipita hapa na pale katika makundi ya watu, hakufanikiwa kumuona Yule binti. Ikabidi aulize, kila mtu akamwambia hajamuona. Joru akiwa amekata tama ya kumuona akarudi alikowaacha Mama Shibagenda na watoto wake, wakaungana tena.

    “Ulienda wapi?” mama Shibagenda akauliza.

    “Nilikuwa namwangalia Yule msichana aliyenifata na motto, nahisi motto Yule ni wangu, bila shaka,” Joru alimueleza mama Shibagenda.

    “Kumbe Joru ulikuwa Simba mwenda pole ee?” mama Shibagenda alizungumza huku akitikisa kichwa chake.

    “Aaaa mama ni stori ndefu, siku tukitulia nitakusimulia” Joru alieleza.

    “Ok, basi uwe unauliza kwanza, yuko pale ndani ya gari ananyonyesha motto, atakuja,” mama Shibagenda alimwambia Joru. Joru akamtazama na kucheka, akainua chupa ya sodana kujimiminia. Japokuwa Joru alikuwa na wenyeji wake hao bado pongezi nyingi zilikuwa zikimiminika kutoka kwa kila aliyepita na kumuona hapo. Dakika chache baadae Yule binti akaja pale walipo, Joru akainuka na kuwahi kumpokea mtoto, akambusu na kisha kumbeba begani, akamkumbatia na Yule binti naye akambusu.

    “Koku!” akaita, “Samahani kwa kila kitu, zilikuwa ni silka za ujana na mambo yake,” Joru aliomba msamaha kwa Koku kwa lile alilolifanya takribani mwaka mmoja uliopita.



    “Usijari Joru, nilikwishakusamehe muda mrefu sana na kila siku nilikuwa naomba Mungu nikutane nawe nikupe mtoto wako, mi nimeshazaa inatosha,” Koku alijibu.

    “Una maana gani unaposema hayo?” Joru aliuliza.

    “Mimi nimeshachumbiwa na mtu mwanaume ninayempenda, hivyo siwezi kuwa nawe tena, mchukue mwanao na mi nikaanze maisha mapya,” Koku alijibu huku akiondoka. Joru alimtazama Koku akiondoka na kumuwacha na mtoto mikononi mwake, Joru akarudi na kumkabidhi mama Shibagenda Yule mtoto.

    “Vipi?” mama Shibagenda akauliza huku akimpokea Yule mtoto.

    “Ameniachia mtoto yeye ameondoka,” Joru akajibu huku akiangusha machozi.

    “Usijali mwanangu, tutamlea tu, atakuwa bila tabu, nitatafuta binti atamwangalia mtoto,” mama Shibagenda alimfariji Joru na kumtuliza.

    Shughuli zote zilikamilka na watu wakatawanyika. Mama Shibagenda akaondoka na Yule mtoto, Joru akabaki kambini kwa siku mbili zaidi kabla ya kurudi nyumbani.



    7 …baada ya siku mbili.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    WAHITIMU wote wa mafunzo walipangiwa vituo vyao vya kazi, walitakiwa kuripoti baada ya wiki mbili za mapumziko. Haikuwa hivyo kwa Joru, yeye hakupata taarifa yoyote ya kuripoti kazini. Alibaki kama alivyo, ‘Labda nitabaki hapa hapa,’ alijiambia mwenyewe. Siku hiyo alikuwa akifungafunga begi lake tayari kwa safari ya kurudi nyumbani kwa Shibagenda, kichwa chake kilikuwa kina mambop mengi kiasi yaliyokuwa yanakinzana, mojawapo lilikuwa ni juu ya Yule mtoto aliyeachiwa, jinsi gani ya kumlea, lakini aliamini kuwa kama yeye alibaki bila mlezi tangu umri wa miaka kumi mpaka siku hiyo basi vivyo hivyo na mtoto huyo ataleleka. Joru alitoka nje na begi lake mkononi, akakutana na MP mmoja akija kwenye bweni lao.

    “Joru, unatakiwa ofisini mara moja,” Yule MP alimpa ujumbe kisha naye kuondoka zake, Joru alielekea ofisini kama alivyoambiwa, aligonga na kuingia katika ofisi hiyo nadhifu, ofisi ya mkuu wa kikosi. Akasimama imara na begi lake mgongoni akapiga mguu chini na kutoa heshima ya kiaskari. Yule mkuu naye akajibu.

    “Nimeitika wito mkuu,” Joru aliongea huku akiwa kasimama kikakamavu, kiaskari kwelikweli.



    “Joseph Rutashobya, najua umejiuliza kwa nini hujapangiwa kituo kama wengine, usijali, kwanza kabisa jeshi limekutazama kwa jicho la pekee sana, kama askari mkakamavu, mpiganaji, mvumilivu asiyekubali kuishindwa, hivyo umependekezwa kuendelea na mafunzo zaidi. Hapa tunavyoongea unatakiwa kuondoka leo hii kuelekea Chukwani, Zanzibar kwa mafunzo mengine ya miezi sita katika medani za kivita katika ngazi kubwa zaidi. Huna muda wa kupumzika wala huna wa kumuaga, nimemaliza, unaweza kwenda,” Yule mkuu wa jeshi alimaliza. Joru alirudi nyuma hatua moja na kuptoa heshima ileile akageuka na kutoka nje, pale akakutana na askari mwingine.

    “Samahani we ndio Joseph Rutashobya?” akauliza.

    “Ndio afande,” Joru akajibu.

    “Ingia kwenye gari tuondoke haraka, tumechelewa,” akaambiwa. Ukiwa jeshini hakuna lele mama lazima kuwa tayari muda waote. Joru akakwea gari na ile gari ikaondoka katika kikosi cha Mtukula.

    Ndani ya masaa mawili Joru alikuwa katika dege la jeshi Buffalo akielekea Dar es salaam. Ilikuwa ni mara ya kwanza Joru kupanda ndege, mara ya kwanza Joru kutoka nje ya mkoa wa Kagera, kwake ilikuwa kama anayeota ndoto, lakini hili hakika ndilo alilokuwa akilitaka siku zote.

    Joru alikuwa mwanajeshi, mwanajeshi aliyeonekana kati ya wote aliokuwa nao, waliochaguliwa kwa vyeti vyao, lakini yeye ukakamavu na uvumilivu wake ulimpeleka mbele zaidi.



    §§§§



    Nyumbani kwa Shibagenda walipigiwa simu tu kuwa Joru hatorudi nyumban mpka baada ya miezi sita, mama Shibagenda alisikitika sana ukizingatia alikuwa ameandaa chakula kizuri kwa ajili ya kijana wao waliyempenda sana, Joru.

    Maisha yaliendelea, mama Shibagenda alipata msichana wa kumlea Yule mtoto, hakuwa msichana mdogo bali mwanamke mwenye umri kama miaka 28 na 32 hivi lakini alikuwa bado kuolewa, walikutana sokoni ndipo alipoongea nae baada ya kutambulishwa na mwanamama mwingine.



    Msichana Yule alijitambulisha kwa jina la Kemilembe, na moja kwamoja alikuja kuishi kwa mama Shibagenda, naye alipotambulishwa mtoto jina lake Joseph Rutashobya, moyo wake ulipaa kwa mshtuko, akamkumbuka Joseph wake waliepoteana zaidi ya miaka ishirini ilopita. Kemi alimlea kwa upendo mkubwa sana mtoto Yule, kwani alikuwa akimkumbusha mbali sana.

    Kemilembe wakati yakitokea yale mauaji pale kijijini kwao, yeye na wazazi wake walitoroka usiku ule ule na kwenda kijiji kingine, hilo ndilo liliwaweka hai. Daima alimkumbuka rafiki yake Joseph waliekuwa wakienda pamoja shuleni, wakicheza njiani, wakiwekeana ahadi mbalimbali za maisha ya baadae, lakini mawazo hayo yote alijaribu kuyafukuza na kusema ‘ulikuwa utoto,’

    Siku zikapita, miezi ikayoyoma, Kemilembe akawa mlezi mzuri sana kwa mtoto Joseph, mtoto huyo akakua kwa kimo na akili, akajifunza kutembea, akajifunza kuita ‘mama’ akimwita Kemilembe kwa jina hilo, naye Kemi alikuwa akiitika na kufurahia kuitwa hivyo, kwani ni Baraka ya pekee ambayo wengine wachache hawaipendi ndio maana hutupa watoto, wakisahau kuwa hilo ni tendo la dhambi, tena dhambi kubwa.



    §§§§



    ….Miezi sita Baadaye

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Joseph Rutashobya ‘Joru’, alimaliza awamu ya kwanza ya kozi ngumu kuliko maelezo. Walikwenda vijana sitini lakini waliomaliza salama walikuwa arobaini na tano, watano kati yao walipoteza maisha, wengine waliishia njiani kwa sababu mbalimbali, lakini bado Joru alionekana kuwa mahiri katika mafunzo hayo, ya kuruka kwa miamvuli na kutua katikati ya bahari, kuogelea umbali mrefu na kukaa ndani ya maji kwa muda mrefu ikiwa ni mbinu ya kujikinga na maadui inapobidi.

    Joru alisifiwa na kila mkufunzi hasa wale waliotoka nje ya nchi kama Urusi na Umarekani, walimpenda kijana huyo na wenzake wawili ambao walionekana pia kuwa mahiri kwa namna Fulani. Baada ya miezi hiyo sita, walitakiwa kurudi mapumziko ili wasubiri taarifa nyingine kutoka kambini. Joru na wenzake walirudi mpaka Dar es salaam na kufikishwa moja kwa moja katika kambi ya Makongo (Lugalo Barracks).



    Baada ya siku nyingine tatu Joru alipata ruhusa ya kwenda kusalimia kwao Mtukula. Aliamua kwenda bila kutoa taarifa kwa mtu yeyote, kesho yake tu tayari alikuwa Kagera kwani alifanikiwa kupata ndege ya jeshi inayokwenda huko. Jioni ya siku ya tano alikuwa akielekea Mtukula, nyumbani kwa jenerali Shibagenda, maana huko ndiko kumekuwa nyumbani kwake sasa.

    Hodi iliyogongwa katika mlango wa mbele wa nyumba ya Shibagenda iliwagutusha wote waliokuwa sebuleni wakiangalia TV, aliyetoka kwenda kufungua mlango alikuwa ni mama Shibagenda mwenyewe, hakuamini anchokiona mbele yake, hakuamini kama Joru ndiye aliyesimama mbele yake, alimkumbatia kwa bashasha, akampokea begi lake na kumkaribisha ndani, watoto wa shibagenda waliokuwa hapo sebuleni nao walikuwa na furaha ya ajabu kumkaribisha kaka yao waliyemzoea kwa miaka mingi, walimkaribisha sebuleni, naye akaketi kitini.



    “Mwanangu yuko wapi?” lilikuwa swali la kwanza kuuliza.

    “Aaaa jamani Joru hata hujapumzika?” Mama Shibagenda akajibu.

    “Hapana, yeye ndiye hasa nilikuwa namfikiria katika safari yangu yote,” Joru akajibu. Mama shibagenda akamwita Kemi kwa sauti ili aje kumleta mtoto amsalimie baba yake. Joru akiwa anafungua kamba za buti zake alihisi nywele zikimsisimka akatazama chini akaona kuna mtu aliyesimama, akamtazama, mtoto wa kiume.

    “Waoh!” Joru akamnyanyua, “Sikujua hata kama ni wa kiume au wa kike, sasa mnamwita nani?” akauliza.

    “Joseph Rutashobya, junior,” mmoja wa watoto wa Shibagenda akajibu. Mara Joru akainua macho kumtazama dada anayemlea mwanawe, lo! Akagongana macho na Kemilembe, Kemilembe yuleyule aliyekluwa akishikana nae mikono kwenda na kurudi shule, Joru alibaki kama aliyenaswa kwa umeme. Walibaki wakitazamana, nyumba yote ikawa kimya, Kemi akamkumbatia Joru kwa nguvu, Joru akaonekana kufurahi bila kuficha.



    “Kwani nyi mnafahamiana?” mama Shibagenda akauliza.

    “Mama, sisi tumetoka mbali sana, mimi nilijua Kemi inawezekana hata alishakufa, maana nilipoondoka pale kijijini miaka ile ndipo sikumwona tena!,” Joru alimwambia mama Shibagenda, alirudisha kumbukumbu yake mbali sana, Kemilembe aliangusha machozi kwa maana hakutegemea kabisa kama angemuona tena mwanaume huyo aliyeahidiana nnaye kuishi kama wazazi wao wakiishi, sasa wamekutana tena katika umri wa utu uzima.

    “Kemi, ulikuwa wapi siku zote hizi?” Joru alimuuliza Kemi, Kemi akamtazama Joru, jicho lake lilizungumza lugha iliyojificha ‘nakupenda Joru’. Joru alimtazama mwanawe kisha akamtazama Kemi, hakika katika siku zote hizo Joru aliishia kulia tu kila alipomuwaza Kemi.



    rejea 1977˜

    Kijijini kwa kina JORU na KEMI



    USIKU HUO wa uvamizi, Kemi alikuwa amelala ndani ya nyumba yao, akiwa hana hili wala lile, ndoto tamu za maisha zilikuwa zimeugubika usingizi huo ambao siku hiyo haukuwa na mang’amung’amu bali ulikuwa ni usingizi mzito, Kemi alilala fofofo.

    Ngurumo za magari ziliposikika, wazazi wa Kemi hasa baba yake , alishtuka kutoka usingizini, aksikiliza mlio huo, akahisi ukija upande huo, baba wa Kemi akamuamsha mkewe, akamwambia asikilize gari hilo, mlio ulizidi kuongezeka.

    “Baba Kemi, hapa sio pa kukaa tena,” Mama Kemi akamwambia mumewe.

    “Umeona ee?” Baba wa Kemi akajibu, akavuta kapazia na kuchungulia nje, akaona mwanga wa magari hayo ukisogea pale kijijini.

    “Muamshe Kemi, muamshe haraka!” Baba Kemi alimwambia mkewe. Mama Kemi hakusubiri hata kauli ya mumewe ifike mwisho, tayari alikuwa katoka chumbani na kumuendea binti yake.

    “Kemi, Kemi, Kemi,” alimuamsha kwa kumtikisa, Kemi ndio kwanza alijigeuza upande wa pili. Ilikuwa taabu kidogo kumuamsha Kemi, hakukuwa na jinsi alimtikisa kwa nguvu na kufanikiwa kumuasha.

    “Mama nini jamani, mbona hakujakucha?” Kemi aliongea kwa sauti ya uchovu uliojaa usingizi, mama yake akamnawisha maji usoni, fahamu zikamjia sawasawa.



    “Wamekuja kutuvamia watatuua, tuondoke” mama yake alimwambia huku akimvuta mkono binti yake na kumtoa chumbani, kisha wakasubiri kwenye kikorido. Baba wa kemi akatangulia mlango wa kutokea nyuma akiwa na kurunzi yake mkononi, akausukuma taratibu na kutazama nje huku na kule, ni mbala mwezi tu iliyokuwa iking’aa kila upande, akamvuta mwanawe na mkewe na kuvuka upenuni mwa ua wa nyumba yake, hakujali hata kama alikuwa akisikia sauti za wavamizi ambao tayari walikuwa wameshuka katika magari yao na kuanza vurugu zao. Kemi na wazazi wake walifanikiwa kujificha katika mapori ya migomba na kupiga jicho kinachoendelea, walishuhudia watu hao wakifungua mazizi ya mifugo yao na kuiswaga kwenda garini. Baba wa Kemi aliumia sana kwa hilo mara kadhaa alishikwa na hasira akataka kujitokeza kwenda kupambana na watu hao, lakini mkewe alimkataza, akimuhasa kuwa atauawa ni bora aache. Mara kelele za akina mama na watoto zikawa zinasikika.



    “Mama Joru yuko wapi?” Kemi akauliza.

    “Joru yuko kwao!” mama yake alimjibu kwa kifupi tu.

    “Mama nendeni mkamchukue Joru, masikini watampiga,” Kemi akaanza kulia kwa uchungu. Alikuwa ni binti mdogo wa miaka kumi tu, lakini mapenzi aliyoyaonesha kwa mtoto mwenzie, Joseph Rutashobya, yalikuwa ni mapenzi mazito. Mama yake akambembeleza akimwambia kuwa Joru ni mtundu kwa vyovyote atafanikiwa kutoroka. Kemi alitulia, akiamini kabisa yote aliyoambiwa na mama yake yana ukweli mwingi. Mara wakaanza kusikia milio ya risasi ikitokea upande wa pili na kelele za watu zikisikika. Baba wa Kemi akamshika mwanae na mkewe akaanza kuwavutia maporini ili wasionekane, akawapeleka umbali kidogo na kuwaficha kwenye vichaka, kisha yeye akarudi kushuhudia nini kinaendelea, ndipo alipokuwata nyumba yake ikiteketea kwa moto, vilio vya huku na kule, akashuhudia wavamizi haop wakiwapiga wananchi na wengine wakibaka wanawake. Aliumia sana lakini hakuwa na la kufanya, akaamua kuondoka na kwenda alikoiachafamilia yake, akawachukua na kupotelea msituni.



    Baada ya siku mbili tangu yale yatokee, mzee Yule alirudi kutazama hali ya kijiji kile, alilia sana, hakukuwa na nyumba iliyobaki, majivu yalitapakaa kila mahali, aliwaona kwa mbali vijana wa JW waliokuwa wakihifadhi miili ya marehemu huku eneo lile limefungwa utepe maalumu wa kuzuia kuingia. Baba wa Kemi akageuza alikotoka, akatembea hatua chache na kusimama akageuka na kuangalia kijiji chao walichokipenda, hakujua nani na nani waliokufa katika sakata hilo wala hakujua nani na nani waliopona, akaendelea na safari yake.

    Siku zilikwenda na wiki zikapita, Kemi alitamani sana kumuona Joru lakini haikuwa hivyo, kila siku alikuwa akiomba kumuona Joru lakini wapi. Kutokana na umbali wa makao mapya, Kemi alianza shule nyingine na kuendelea na masomo yake, hakuwa na raha kila alipokuwa akienda shuleni. Wakati vita ya Tanzania na Uganda ilipopamba moto miaka ya 1978 mpaka 1979 Kemi alitamani siku hizo angemuona Joru. Kwa kuwa alijua wazi Joru alikuwa hampendi kabisa Idd Amin tangu wakiwa shuleni, na marakadhaa alipokuwa akiwaona wanajeshi siku zile wakiwa mazoezini Joru alikuwa akishangilia sana.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Hakukuwa na jinsi, wazazi ilibidi wamuelekeze Kemi kuwa Joru atakuwa amekufa katika siku ile ya uvamizi, Kemi alilia sana kwa habari hiyo, alimlilia sana Joru lakini kwake ilikuwa ngumu kuamini, yeye kwa umri wake alijuwa wazi kuwa wanaokufa daima ni wakubwa tu na si watoto. Mwaka 1984, baba wa Kemi akafariki baada ya kuumwa sana, alifariki kwa maradhi ya UKIMWI; Kemi akabaki na mama yake tu, ijapokuwa maisha yalikuwa ya tabu kidogo lakini waliweza kusonga mbele. Bado moyoni mwa Kemi aliamini kabisa kuwa ipo siku Joru ataonekana mbele ya macho yake. Kemi akawa msichana mkubwa na mrembo sana, kila mwanaume alimtamani msichana huyo kwa jinsi alivyoumbika, sura, rangi, umbile, vyote vilimfanya Kemi kuonekana msichana mrembo pote kijijini. Wazee wenye watoto wa kiume walio tayari kuoa walikuja kuongea na mama Kemi na ndugu wengine wa familia hiyo ili kumposa binti huyo kwa vijana wao, lakini kila ilipoamuriwa hivyo, Kemi alitoroka nyumbani. Aliapa kuwa penzi lake si kwa mwanaume mwingine ila Joru tu, awe hai au amekufa, Kemi alijiwekea hilo moyoni na alishawahi kumweleza mama yake kuwa yeye alipenda kuolewa na Joru pekee, hivyo atabaki kuwa hivyohivyo mpaka mwisho wa maisha wake, hakika Kemi alijitunza na akatunza kila alichonacho kama nadhiri yake ilivyokuwa. Kemi alifanikiwa kufika kidato cha nne, lakini hapo hakuweza kuendelea kutokana na hali ya afya ya mama yake. Mama yake alikuwa akiumwa sana, alikonda sana na hakukaa muda mrefu alifariki mikononi mwa Kemi mwaka 1987.



    Baada ya msiba huo kumalizika, Kemi hakuona haja ya kuishi kwa ndugu yeyote, aliamua kuchukua maisha yake mikononi mwake, akaondoka kijijini hapo na kuhamia mjini ambako hakuwa na ndugu yoyote, akatafuta kazi akapata kwenye familia ya kiarabu iliokuwa ikiishi Bukoba mjini, mji ambao Joru alishafanya fujo zake na kuondoka miaka kenda nyuma na kutorokea mahali pengine.

    Kemi alifanya kazi na vibarua mbalimbali kwa miaka kadhaa mpaka alipoamua kurudi tena Mtukula, huko akawa akiishi kwa mama Fulani na kumsaidia kuuza mboga katika soko la Mtukula. Maish aliyokuwa akiishi yalikuwa ya taabu sana, wakati mwingine alikuwa akishinda bila kula, lakini kwake haikuwa na jinsi angeenda wapi, uzuri Kemi ulichujuka sana kutokana na lishe duni ya hapo alipokuwa akiishi, mama aliyekuwa akiishi nae alikuwa hamjali, alipenda amfanyie kazi tu, maana tangu ampate Kemi alikuwa na soko kubwa sana la mboga zake kwani watu wengi walipenda kununua mboga kwa Kemi kutokana na lugha safi kwa wateja wake. Hata mama Shibagenda daima alikuwa akiishia kwa binti huyo kununua mboga.



    Baada ya miaka kadhaa kupita

    §§§§§



    Nyumba aliyokuwa akiishi Kemi, kwa mama mboga kulikuwa na kijana wa kiume aliyekuwa akimpenda sana Kemi, kila mara alimtongoza, alimshawishi kufanya naye mapenzi lakini Kemi alikuwa mgumu haswa. Yule kijana hakukata tama kwa maana alikuwa akienda mtaani vijana wenzie wakimcheka kwa kuwa alikuwa na msichana ndani na alishindwa kufanya chochote, hii ilimtia hasira sana, siku moja akapania kumbaka Kemi ikiwa atakataa kumtimizia haja yake.



    Ilikuwa purukushani usiku huo katika chumba cha Kemi, Kemi hakukubali kijana huyo amfanyie hilo atakalo, katika vuta nikuvute hiyo Kemi alimgonga kichwani kijana huyo kwa kutumia mfuniko wa chungu, Yule kijana akaanguka na kupoteza fahamu, kisha Kemi akaona hapo sio pa kukaa tena, alitoka nje usiku huo na kutoroka. Usiku huo mama mboga alikuwa akisika fujo zote hizo lakini hakufanya lolote kwani kijana wake alishamwambia kuwa yeye lazima ampate Kemi hata kwa kumbaka na mama yaek alimruhusu kufanya hivyo kwa binti huyo yatima. Lakini baada ya kama dakika kumi na tano alisikia kitu kikianguka na ukimya ukatawala isipokuwa mlango wan je uliofunguliwa na kufungwa. Wasiwasi ukamjaa mama mboga ikabidi aende kutazama akijua labda tayari shughuli inaendelea, chakushangaza hakusikia hata miguno ya mahaba ambayo alikuwa akiisubiri kwa hamu. Lo, kusukuma mlango tu anakutana na mwili wa mwanae ukiwa chini uchi wa mnyama, hakujua kama kazimia au kapoteza maisha, akaanza kulia kwa sauti na kuita majirani. Dakika tano tu zilitosha majirani kujaa, balozo wa nyumba kumi akafika na kuona hali hiyo, wakaita polisi wakatazama na kuandika ripoti zao, kijana alikuwa amekufa kwa kuwa amechelewa kupata huduma ya haraka.



    RB ikatolewa, Kemi atafutwe popote alipo ili sheria ichukue mkondo wake. Mkono wa dola ni mrefu, Kemi alikamatwa baada ya siku tatu, akarudishwa Mtukula, kesi yake ikaunguruma na kuwavuta karibu watu wengi wa Mtukula, Kemi alipata mashahidi wengi sana kumtetea. Baada ya miezi miwili jaji aliyekuwa akiendesha kesi hiyo akaridhika na ushahidi uliotolewa, maana ilionekana wazi kuwa marehemu amefia katioka chumba cha binti tena akiwa mtupu, usiku wa manane, kelele za fujo hiyo kwa vyovyote ingemuamsha mama mboga lakini kwa nini hakuamka, ilikuwa njama. Hukumu ikatolewa Kemi akafungwa miaka miwili kwa kosa la kuua bila kukusudia, japokuwa alifungwa lakini wanakijiji waliona ni heri miaka hiyo miwili kuliko kufungwa maisha. Msamaha wa Rais ulipotoka, Kemi akaangukukiwa na bahati hiyo akatoka gerezani baada ya kukaa miezi sita tu. Kemi akarudi na kuanza maisha mapya kabisa, bado moyoni mwake alikuwa akiomba japo hata kwa ndoto Joru aje atoe usichana wake kwanza hapo labda angemfikiria mwanaume mwingine, daima alishinda akilia, hakupenda kuchangamana na watu.



    Siku moja katika usingizi wake akamuota Joru, akaota kuwa kakutana na Joru sokoni, na kupeana ahadi zao zilezile za tangu utoto, ‘tutaishi kama baba na mama wanavyoishi’. Aliamka mwenye furaha sana, alipojiswafi asubuhi hiyo aliamini kabisa kuwa atakutana na Joru sokoni, aliokwenda sokoni asubuhi na kushinda huko akizungukazunguka mara akiongea na huyu mara na yule, kila aliyemjua binti huyo mwenye huzuni siku hiyo alishangaa kumuona akiwa na furaha ya ajabu. Saa zilikwenda lakini Kemi hakumuona Joru, ilikuwa ni ndoto tu, ndipo alipotoka na kuketi pembeni mwa soko hilo karibu kabisa na barabara. Mara akasikia sauti ikimwita, akageuyka na kumuona mwanamke aliyemzoea, mama Shibagenda, wakafanya mazungumzo mawili matatu, akamchukua na kuja naye nyumbani ili amsaidie kulea mtoto wa Joru. Kemi alipigwa na butwaa aliposikia kuwa mtoto huyo anaitwa Joseph Rutashobya, alimlea kwa upendo mkubwa akilala nae kitanda kimoja kana kwamba ni mtoto wa kuzaa mwenyewe.



    §§§§§

    Rejea JORU na KEMI



    JORU alimkumbati Kemi kwa nguvu, wote wawili waliangusha machozi. Mama Shibagenda alibaki kuwaangalia vijana hao. Wakati wakiwa katika kukumbatiana huko Kemi alihisi mwili ukimtekenya sana, alihisi raha ya ajabu, alizidi kumkumbatia Joru. Baada ya dakika kama tano za kumatiano hilo, Joru alimuachia Kemi, akamfuata machozi.

    “Ina maana ninyi mnafahamiana?” Mama Shibagenda akauliza.

    “Mama tunafahamiana tangu utoto wetui, tumelelewa kijiji kimoja na tulikuwa marafiki wa kweli, sikutegemea kama mrembo wangu yuko hai,” Joru akaeleza, ndipo mama Shibagenda alipopata kujua mkasa mzima wa Joru na Kemi kila mtu kwa upande wake.

    “Poleni, sana sasa mmeamini kuwa milima haikutani ee? Haya basi Joru, kama kawaida nyumba yako ipo daima inakusubiri, ukajipumzishe kidogo,” mama Shibagenda akamwambia Joru, kisha akamgeukia Kemi aliyekua akionekana na aibu kidogo, “Nani, Kemi! Mchukulie mzigo umuongoze, usijali ni siku nyingi hamjaonana basi mkaongee vizuri na kusalimiana, kazi za huku mi nitafanya tu,” alimaliza mama Shibagenda, Kemi akamchukua begi la Joru na kuelekea kule kunako nyumba ya uani, wakimuacha mtoto akirudishwa kulala…





    Kama kuna kitu ambacho Kemi alikuwa akikifikiria kitafika lini na vipi ni hicho, tangu avunje ungo hakuwahi kukutana na mwanaume. Upendo wake wa kweli kwa Joru ulimfanya Kemi kuuhifadhi usichana wake mpaka huyo aliyetamani kumpa afike, ijapokuwa alikuwa hajui kama yupo hai au amekwishakufa, lakini upendo wa kweli ulimwongoza katika hili. Kemi alikuwa mtu wa kuweka ahadi bila kuvunja, alimpenda Joru, alimpaenda sana, siku zote alikuwa akimfikiria kijana huyo, haja yake hata kama asipoolewa na Joru lakini Joru awe wa kwanza kufungua njia hiyo inayotamaniwa na wengi.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Walifika kwenye nyumba ambayo Joru alikuwa akiitumia tangu kwanza, akakuta kila kitu kipo kama kilivyo.

    “Hapa ndio kwako?” akauliza Kemi.

    “Ndiyo, nyumba hii nilikabidhiwa na baba mwenye nyumba, mzee Shibagenda, niishi muda wote wa maisha yangu, wamekuwa kama wazazi kwangu, wamenipenda kwa upendo wote. Kemi nalikutafuta sana katika nafsi na moyo wangu nisikuone, hakika nilijuwa kuwa labda umekufa miaka ile ya mauaji yaliyotokea pale kijijini,” Joru alimjibu Kemi na kuongezea na mazungumzo mengine. Kemi akatua begi chini, akamtazama kijana Yule aliyekuwa ndani ya sare nadhifu ya jeshi, aliyejaa katika umbo la kiuwanaume haswa, kemi akainamisha uso wake hakupenda kumwangalia usoni.





    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog