Search This Blog

Sunday 22 May 2022

HATI FEKI - 1

 





    IMEANDIKWA NA : HASSAN S. KAJIA



    *********************************************************************************



    Simulizi : Hati Feki

    Sehemu Ya Kwanza (1)





    ***KIDOKEZO***



    JOHN AMIGOLAS YUKO MAHABUSU BAADA YA KUKUTWA AKIWA NA MWILI WA MFANYABIASHARA MAARUFU, GULAM, MARA BAADA YA KUPIGWA RISASI NA MAJAMBAZI AMBAO WALIMVAMIA NA KUCHUKUA PESA ZAKE ZOTE NA KUKIMBIA NAZO HUKU WAKIMPIGA RISASI NA KUMUUA. JOHN ANASHIKILIWA NA POLISI.



    ENDELEA

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    ASUBUHI ya siku hiyo John alikuwa amesimama peke yake.nywele zikiwa timtim huku amepauka baada ya muda mrefu wa kutokuoga na mgomo wa kutokujishughulisha na chochote hadi atakapopata hatma ya jambo lililomleta hapo.



    Mawazo yalikuwa yakimwandama baada ya usingizi wa mang’amung’amu ambao alikuwa hajauzoea. Hakuna aliyejali. Labda kwa kuwa hawakupewa taarifa juu. Juu ya hali aliyonayo. Hakuna aliyejua ni nini kilichomkumba.



    Alipiga ndoo teke. Ndoo iliyokuwepo karibu na sehemu aliyokuwa amelala. Sababu za yeye kuwepo hapo pamoja na ndoo havikumwingia akilini. Alivuruga kitanda na kukaa chini huku akiwa ameshika kichwa chake.



    Hasira zilikuwa zimempanda sana John ambaye alikuwa mahabusu kwa wiki moja sasa bila ya kupewa dhamana. Aliumia zaidi baada ya kuona hakuna msada wowote na kwamba alidhaniwa kwamba yeye ndiye aliyemuua mfanyabiashara mmoja wa magari.



    Hiyo ni baada ya polisi kumwona yeye kwani ndiye aliyekutwa katika eneo la tukio pasipo kuwepo mtu mwingine. Eneo ambalo damu zilikuwa zimetapakaa baada ya watu wenye silaha kumvamia mfanyabiashara aliyekuwa tayari amekufa akiwa amelala chini.



    Mfanyabiashara huyo, Gulam alikuwa akielekea benki kuweka fedha zake na mara alijikuta akiishia mikononi mwa watu wanne waliokuwa na bastola. Walimvamia na kumwibia hela zote na kisha kumuua. Watu hao walifanikiwa kukimbia na gari yao aina ya Mark II pasipo kukamatwa.



    Katika kuwahi kumwokoa, John alikuta yule mfanyabiashara tayari ameshakata roho. Alijaribu kuwaita watu ili kusaidiana lakini baada ya mlio wa risasi kusikika watu walitawanyika na hivyo John alibaki pale peke yake hadi polisi walipofika dakika chache.



    John alikuwa na bastola yake ambayo aliitoa mara tu baada ya kusikia mlio ule na kuishika. Hali hiyo alipelekea polisi kumkamata kwa kumshukia kwamba ni yeye aliyefanya mauaji yale baada ya kukutwa.



    Bastola aliyokuwa nayo alikuwa akiitembea nayo siku zote kwani alikuwa na kibali cha kuimiliki. Wakati wa tukio hakuweza kuonyesha kibali na hivyo alifungwa pingu katika mikono yake.



    Sasa aliishia mikononi mwa polisi kwani majambazi wale walifanikiwa kutoroka na pesa za mfanyabiashara yule. Alijaribu kujielezea kwamba siye yeye aliyefyatua risasi ile lakini polisi hawakumwelewa. Alipelekwa kituo cha polisi cha kati kwa ajili ya mahojiano na kupisha uchunguzi.



    Gari lake aina ya Land Cruiser V8 liliachwa karibu na benki ambapo mauaji yalitokea. Hakujali na wala hakuwajulisha ndugu zake walifate. Aligundua kwamba alikuwa amelifunga vizuri na hivyo alielekea polisi.





    *****

    John hakujua lililoendelea nyumbani kwao kwani alijua si rahisi ateseke mahabusu wakati Mzee wake anaweza kumwekea dhamana akawa huru. Akiwa bado kituoni ndani, siku inayofuata alipata taarifa juu ya kifo cha Mzee wake Amigolas. Baba yake mzazi. John alichanganyikiwa sana hadi kupoteza fahamu.



    Hakuwa amemini kama ni kweli baba yake amefariki dunia. Baadhi ya askari walimsaidia kumpepea hadi akazinduka, alizinduka akiwa hajitambui vizuri. Bado alikuwa haamini kama ni mzee Amigolas aliyefariki.



    "Amigolas, baba... Amigolas...baba," ndio majina yaliyokuwa yakitajwa na John siku nzima. Hakujua juu ya familia yake kwani taarifa zilizokuja zilikuwa za baba yake kuuliwa.



    Polisi walimwonea huruma lakini asingeweza kuachiwa kwenda kuona hadi uchunguzi wa tukio lake utakapokamilika.



    Hakuna mtu aliyejua lolote kuhusu John kwani siku hiyo ndo siku ambayo nyumbani kwa kina John palipata pigo kubwa sana. Ni siku hiyohiyo John alikuwa aachiwe huru baada ya uchunguzi kuonyesha kuwa si yeye aliyeua.



    “John aachiwe huru,” mkuu wa kituo alitoa kauli hiyo baada ya kupiga simu na kuongea na Afande Mushi.



    "Naomba hilo file la John Amigolas, anatakiwa aje aweke saini. Na umtoe huko ndani. Taarifa kutoka kwa mkuu zinasema kwamba si yeye aliyeua. Afande Nicco, kamtoe huko aliko umlete hapa," Afande Mushi alitoa amri na kusisitiza kwa afande Nicco ambaye alileta faili la John na kwenda kumtoa. Alikabidhiwa vitu vyake na kuruhusiwa japo alikuwa akionekana kutojitambua.



    Alitoka nje ya Kituo cha polisi. Aliangalia uelekeo na kwanza alitaka kulifuata gari lake. Alitaka kujua ni kina nani waliotekeleza mauaji kwa baba yake na ni kwa sababu gani. Gari lake lilikuwa limeshaletwa hadi kituoni. Aliingia na kuwasha.



    Aliifuata Barabara ya Uhuru kuelekea Hospitali ya Mount Meru, hospitali kubwa jijini Arusha. Alijua kwamba mwili wa baba ake utakuwa umehifadhiwa huko. Hakutaka hata kurejea kwanza nyumbani kwani angechelewa kupata uthibitisho kwa kuona kweli mwili uliopelekwa hospitali ni wa baba yake Mzee Amigolas.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Alifika hospitali na kukuta umati wa watu ukiwa unafuatilia juu ya maiti zilizoingizwa hospitalini hapo asubuhi. Alisikia tu minong’ono ya watu ambao walikuwa wakisikitika kutokana na kuona maiti zikiingizwa na kupelekwa chumba cha kuhifadhia maiti.



    Alisogea na kukutana na mmoja wa majirani zao ambaye alishirikiana na polisi kuzileta maiti hospitali hapo.



    "Gaudence, ni...ni kweli maiti iliyoletwa ni ya baba yangu, tafadhali naomba niambie, we ni kama ndugu yetu. Tafadhali Bwana Gaudence,” John alikuwa akimuuliza Gaudence ambaye ni mmoja wa majirani zao huku akilia kwani alijua kuwapo tu kwa Gaudence hospitalini hapo kunadhihirisha ya kwamba mzee Amigolas amefariki kweli.



    "Pole sana John, ni kweli na si baba tu, wameuliwa pia ndugu zako pamoja na mama yako Magdalena.”



    "Unasemaje?” John aliishiwa nguvu na kukaa chini huku akilia. Gaudence alimsaidia kumwinua na kumpeleka katika gari lake alilokuwa amefika nalo hospitali.



    “Usilie bwana John. Jikaze….hii ni kazi ya Mungu. Tuko pamoja.”



    “Ina maana na wadogo zangu Isack, Neema na Jenipha?”



    “Ndiyo John, wameshapelekwa chumba cha maiti, tunachosubiria ni taarifa za polisi kama watu waliowaua wanajulikana na itatangazwa pia katika vyombo vya habari baada ya uchunguzi,” Gaudence alimwambia John ambaye muda wote alikuwa amejiinamia huku akilia.



    Aminata alikuwa ameshafika hospitali. Alikuwa anazunguka huku akifatwa na waandishi wa habari, alikuwa akielekea ndani kuonana na daktari mkuu wa hospitali hiyo. Baada ya muda alirudi akiwa anaangaza huku na huko. John alimtazama. Alihisi kukumbuka kitu lakini machungu ya kumpoteza mzee wake hayakumpa nafasi ya kutafakari lililotokea.

    Aminata alimfuata baada ya kujua kuwa ni John. Alimfuata ili kuthibitisha.

    "Habari yako kaka?” Aminata alimsalimia John ambaye alikuwa akimwangalia muda wote.



    “Salama tu dada, karibu,” John alipata picha juu ya Aminata, alikumbuka kwamba alishawahi kumwona akiwa ameongozana na polisi wakati akikamatwa na baada ya hapo hakumwona tena hadi alipoachiwa huru.



    “Inawezekana huyu ni mpelelezi,” aliwaza John huku akimwangalia Aminata aliyekuwa tayari amefika alipokuwa John.



    “John, nadhani ndiyo wewe,” Aminata alimuuliza John jina lake kama kuthibitisha kweli alikuwa ndiye John mtoto wa Amigolas.



    “Yes, ndiyo mimi. Kuna tatizo na mimi dada,” John hakuelewa Aminata alichomaanisha. Ndiyo kwanza ametokea mahabusu na sura ya Aminata aliikumbuka tayari. Hakujua Aminata alikuwa anashida gani na yeye.



    "Nahitaji ushirikiano wako, baada ya kumaliza mazishi naomba unitafute,” Aminata alimaliza kuongea na kuondoka kulifuata gari lake. Aliwasha na kuondoka. John aliachwa na maswali kichwani. Alitakiwa amtafute Aminata baada ya mazishi ya ndugu zake.





    *****

    Taarifa za vifo zilimfikia Antony ambaye alikuwa nchini Kenya. John ambaye ni pacha wake, alimfahamisha na hivyo Antony alipanga kurudi kumzika baba yake pamoja na ndugu zake. Maumivu yalikuwa makubwa sana kuwapoteza.



    Baada ya siku mbili Antony aliwasili akitokea Nairobi nchini Kenya ambako alikuwa akifanya shughuli zake za biashara huko. Mzee Amigolas alikuwa amefungua maduka makubwa ya vitu mbalimbali vya umeme na nguo za kifahari. Maduka hayo yalisimamiwa na Antony.



    Antony aliungana na ndugu zake katika mazishi huku akiwalilia sana. Ulikuwa ni msiba mzito sana kwa John na Antony ambao walibaki wenyewe. Antony alilia sana. Hakuamini macho yake kwa kuwapoteza watu wake wa karibu. Watu wengi walifika nyumbani kwa marehemu Mzee Amigolas. Na hii ni kutokana na kuwa maarufu kutokana na biashara zake.



    Mzee Amigolas alikuwa ni mfanyabiashara maarufu wa madini aina ya Tanzanite. Alimiliki mgodi mkubwa wa madini hayo huko Mererani. Alikuwa ni tajiri mkubwa sana ambaye kutokana na utajiri wake na umaarufu wake, aliweza kushirikiana na matajiri wenzake kusafirisha madini nje ya nchi na kuyauza.



    Utajiri wake ulijulikana kwa watu wengi. Alikuwa amewekeza kwa kujenga nyumba nyingi na hoteli mbalimbali mkoani Arusha pamoja na mikoani kama Dar ea Salaam. Pia maduka makubwa ya biashara nchini nan je ya nchi. Alikuwa ana nyumba kubwa sana maeneo ya Njiro aliyoishi pamoja na familia yake.



    Alimuoa Magdalena na kufanikiwa kupata watoto watano yeye na pacha wake Antony, Isack, Neema pamoja na Jenipha.



    Nyumba yake ilikuwa kubwa sana na yenye ulinzi mkali sana. Alimiliki magari mengi ya kifahari ambayo yalitumiwa zaidi na watoto wake. Watoto wake wawili mapacha John na Antony walikuwa wakisimamia baadhi ya biashara za baba yao. Antony ambaye ndiye aliyekuwa mdogo. Alikuwa akisimamia biashara za baba ake nchini Kenya. Wadogo zao Isack, Neema na Jenipha walikuwa wakisomea nchini Uingereza. Waliishi huko na mama yao Magdalena.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hadi mauti yanawakuta, walikuwa likizo kwa ajili ya sikukuu ya Chrismass na Mwaka Mpya. Hawakuwa na taarifa juu ya kuvamiwa usiku kwani wauaji walianza kuwaua walinzi wawili pamoja na mbwa wao kwa kuwapiga risasi kabla ya kufanikiwa kuingia ndani. Hakuna aliyesikia sauti ya risasi kwani walikuwa wameweka viwambo vya kuzuia sauti isitoke. Na huo ndiyo ukawa mwisho wa kuonana na ndugu zake ambao wote waliuliwa.



    Hakuna taarifa za kukamatwa kwa wahusika japo polisi walikuwa wakiendelea na uchunguzi. Alitaka kumuuliza John kaka yake kama alikuwa akijua lolote linaloendelea kuhusiana na vifo hivyo. Hakujua wazo alilokuwa nalo John kwani alihisi John lazma atakuwa na la kufanya na yeye angetoa ushirikiano.



    “Kaka, unampango gani baada ya haya yote,” Antony alimuuliza John siku mbili baada ya kumaliza mazishi.



    “Dah, bado…ila nawasubiri hao polisi wakamilishe uchunguzi wao.



    Wakati huo John alikuwa akifikiria namna ya kumpata Aminata. John na Antony walianza kufatilia mali za baba yao ili wazirithi. Walizunguka kote na kuongea na watu waliokuwa wameachiwa na kujua maendeleo ya biashara hizo. Walifanikiwa kwenye mali nyingi isipokuwa mgodi wa baba yao.



    Utata ukaanza kugubika kwenye suala la umiliki. Baada ya kifo cha baba yake mgodi ulisimama kufanya kazi. Hakuna kilichoendeshwa na wafanyakazi wote walitawanyika wasijue la kufanya.



    Hata wachimbaji hawakuelewa. Tukio lililowashangaza wachimbaji wote. Baadhi ya watu walifika na kuwaamuru wasitishe uchimbaji wa madini hadi watakapoambiwa. Iliwashangaza sana. Wachimbaji wote walijua kwamba mwisho wao wa kufanya kazi umefika.



    "Mgodi umeuzwa, hahitajiki mtu hapa…..ondokeni,” mmoja wa viongozi wa juu wa kundi la Mosses Ndula, Mbashala aliwapa taarifa. Hali hiyo ilileta sintofahamu huku baadhi ya wachimbaji wakilalamikia.



    “Mbona tusipewe taarifa mapema, mnakuja kutuambia wakati tuko kazini, Mzee Amigolas hawezi kutufanyia hivyo, hata watoto wake hawana roho mbaya hivyo, na kama angekuwa anauza mgodi kweli angetufahamisha mapema na kujua hatma yetu, nyie mnakuja tu mnatuambia mgodi umeuzwa…. nendeni, sisi tuende wapi?" Mmoja ya wachimbaji aliyejulikana kama Mbago, ambaye alikuwa ndiye kiongozi wa wa wachimbaji ambaye anamjua sana bosi wake, Mzee Amigolas na watoto wake alikuwa akipingana na watu waliotumwa na Mosses Ndula.



    "Tuonyesheni basi vielelezo siyo mnatuambia tu kwa mdomo, kama ni uongo je? Siku zote karatasi za uthibitisho zinatangulia….tutajuaje kama nyie ni matapeli." Mbago aliwataka watoe vielelezo ili wapate uhakika wa kile walichoambiwa.



    "Hizo nakala za maelezo hatujaja nazo, ila ukweli ndiyo huo. Mgodi umeuzwa na mnatakiwa mfuate utaratibu uliowekwa. Hakuna chenu hapa. Kuanzia sasa hakuna atakayewalipa,” Hakuna aliyemwelewa. Walianza vurugu. Mbashala na wenzake waliwanyooshea bastola wachimbaji lakini hawakurudi nyuma wala kutetereka.



    Baada ya kuona wanazidi kusogea. Mlinzi wa Mbasha alifyatua risasi moja hewani. Hata hivyo wale wachimbaji walizidi kiusogea huku wakiokota mawe makubwa.



    “Aaagh…mama n’kufaa,” mmoja wa wachimbaji alipiga kelele baada ya risasi nyingine kufyatuliwa na kumpata ya begani. Sasa waliamua kurusha mawe.



    “Nani kakuambia upige risasi.” Mbashala alimfokea Yule mlinzi huku wakiingia haraka kwenye gari na kuondoka. Waliwarushia mawe na kufanikiwa kuharibu kioo cha gari lao.



    Baada ya kufanikiwa kuwafukuza. Mbago aliwaita wenzake wote na kujikusanya kwa ajili ya kikao ambacho kngewasaidia kujua hatima yao katika machimbo hayo.



    “Jamani sikilizeni, naomba tuzungumzie hili jambo," Mbago aliwatuliza wachimbaji ili azungumze nao. Wachimbaji wote walitii na kukaa chini huku wengine wakiwa wamesimama kumsikiliza kiongozi wao. Yule aliyepigwa aliopelekwa hospitali na kuendelea na matibabu.



    “Hili jambo sidhani kama tunakubaliana nalo wote, au siyo jamani?"



    "Ndiyoo!Ndiyooo!" Wachimbaji walijibu kwa sauti za kelele kuashiria kuafikiana na kiongozi wao.



    “Mwenzetu kapigwa risasi. Inaonyesha hawa watu wanataka kutuingilia kwa nguvu bila kufuata sharia. Wote tunaona kwamba hakuna ndugu au motto yeyote wa mzee wetu Amigolas aliyefika kutueleza. Hata hao wasaidizi wake hawajaja. Iweje wachukue tu mgodi. Lazima tujue.”



    “Ndiooo! Ndiooo!” wote walishangilia kauli aliyoitoa Mbago.



    Sasa, mi nadhani si jambo zito sana. Mi n’taenda hukohuko nyumbani kwa bosi n’kajue moja. Kama kuna kazi au hakuna. Sisi tumeajiriwa na kama mgodi umeuzwa walipaswa watuambie. Kwani watoto wa Mzee Amigolas si wapo. Mi nafahamiana na John, mtoto wa marehemu. Nitaenda kwao kuongea naye. Hata yeye anaweza kutusaidia. Kesho nitakwenda kujua moja."



    “Ndiooo!” Haki haitapotea. Tujue mojaaa,” wachimbaji walishangilia baada ya kusikia kauli ya kiongozi wao.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Nitaongozana na Masud na Baraka,” Mbago aliwateua wachimbaji wawili ambao angeongozana nao hadi nyumbani kwa Mzee Amigolas.



    “Tukamjulieni hali mwenzetu aliyepigwa risasi.”



    Polisi walikuwa wameshafika katika eneo hilo. Walihakikisha hali ya usalama inarudi. Mbago alikuwa ameshatoa taarifa polisi juu ya watu waliokuja kuuvamia mgodi na kuwafukuza kazi kwa nguvu. Polisi waliwapa taarifa juu ya mgodi ule. Mosses Ndula alikuwa polisi pamoja na wakili wake. Walikuwa wamepeleka hati ya kuonyesha kwamba kauziwa mgodi na Mzee Amigolas kabla ya kufariki na kwamba umiliki wake ungeanza baada ya miezi sita.





    ****

    John alikuwa njiani akielekea kituo cha polisi cha kati. Hakuwa na taarifa zozote kuhusiana na yaliyotokea Mererani baina ya wachimbaji na watu wa Mosses Ndula. Kichwani kwake alikuwa akifikiria juu ya Aminata. Alitaka kujua ni vipi atampata Aminata.



    Aminata Peter, ni mwanamke aliyesomea masuala ya upelelezi na kuwa moja wa wapelelezi wakuu wa jeshi la polisi. Taaluma yake ilimfanya ajuane na watu wengi ikiwapo kugundua njama mbalimbali za watuhumiwa.



    Kama ilivyokuwa kwa John na Antony, Aminata alipata pigo kama lililowapata baada ya baba yake pamoja na mama na ndugu zake kufariki baada yua kuuliwa na majambazi wakati wakiwa njiani. Tukio hilo lilitokea baada ya kuwekewa mawe makubwa barabarani na hivyo kushindwa kupita na kuvamiwa.



    Baada ya kufanikiwa kuwazuia kupita. Majambazi hao walipora vitu vyao vyote pamoja na kuwafyatulia risasi na kuwaua wote.



    Wakati wa tukio hilo la kusikitisha Aminata alikuwa yuko shuleni. Shule ya bweni na hivyo hakuweza kusafiri pamoja na familia yao. Alilia sana kuwapoteza ndugu zake. Upelelezi ulikuwa ukifanyika lakini matokeo hayakumridhisha Aminata ambaye alikuwa na shauku kubwa sana ya kutaka kuwajua wauaji.



    Baada ya kumaliza kidato cha sita, Aminata alijiapiza kufa na kupona hadi ajue mtandao wa wauaji wale. Ikiwezekana autokomeze kabisa. Hakumwambia mtu mwingine yeyote juu ya mpango wake huo. Alianza msako wake taratibu.



    Alipenda kutoka mida ya usiku ili akakutane na baadhi ya vijana na kuzoeana. Alijua lazima watakuwa baadhi wanaufahamu huo mtandao.



    Kwa mara ya kwanza Aminata anaingia ndani ya himaya ya Mosses Ndula. Anakutana na sura za watu wajuao kazi. Sura za kila aina ya wahuni. Haogopi.



    Anakutana na kijana mmoja ambaye alikuwa anavuta sigara mlangoni. Anamwangalia sana kisha anapita. Yule kijana anamfuata.



    “We nani?” anamuuliza Aminata.



    “Mambo kaka angu, mi naitwa Stellah. Nimeshawahi kukuona mahali mjini karibu na Posta.



    “Inawezekana,” yule kijana aliwaza huku akionyesha kuvutiwa na Aminata. Aminata alikuwa ni mzuri sana na hivyo kila aliyemwangalia alimtamani.



    “Unataka nini huku?” alihoji yule kijana.



    “Nadhani nitakuwa nimepotea njia. Samahani sijui huku ni wapi. Naomba unisindikize niweze kutoka huku. Samahani lakini kaka yangu.



    “Aah, niko kazini hapa…lakini nitakusindikiza uweze tu kutoka hapa.” yule kijana alikuwa ndiye mlinzi wa mlangoni katika ngome ya Mosses ndula iliyokuwa eneo la Kambi wa Fisi. Huko ndiko Mosse alijua kwamba hasingeweza mtu yeyote kujua kinachoendelea.



    “Asante kaka yangu,”aminata alimshukuru yule kaka na kisha alimuuliza jina lake.



    “Naitwa Dula,” alisema yule kijana.



    “Sasa Dula, nitakutafuta siku nyingine basi. Nimependa ulivyonisindikiza. Napenda tuwe marafiki zaidi.

    “Aaah, siamini,” Dula aliwaza huku akitabasamu kwa kutokuamini kama ni yeye. Hakujali kwamba ameacha mlango peke yake na kama atatafutwa na mkuu wake ambaye alikuwa ndani. Alimwacha Aminata akiondoka na kumwachia namba za simu ili wawasiliane.



    Dula alirudi haraka. Alifika mlangoni na kwa bahati nzuri hakuna aliyefika hapo tangu atoke na Aminata. Aliendelea kusimama hapo hadi Mosses alipotoka na kuchukua gari lake na kuondoka pamoja na wapambe wake.



    Aminata alifika nyumbani. Ilikuwa ni usiku wa saa tano. Hakuogopa kutembea mwenyewe. Baada ya kuondoka mitaa ya Kambi ya Fisi. Alichukua teksi iliyompekleka hadi nyumbani kwake Sakina. Alijilaza juu ya kitanda na kuanza kutafakari juu ya kumwingia Dula ili aweze kumwambia kuhusiana na Mosses pamoja na kundi lao wote.





    *****

    Asubuhi alimpigia simu Dula na kumtaarifu kwamba wakutane Café la Azziz.



    “Unapajua hapo.”



    “Ndiyo, lakini ni sehemu hatari sana kwetu sisi hasa ukizingatia na jinsi tunavyojulikana mjini.”



    “Unamaanisha nini Dula? Acha woga, we ni mwanamume. Njoo mjini bana. Huko kwenu mbali.”



    “Ok poa bibie. Nakuja hapo.” “kumwacha mtoto mzuri kama yule…ni sawa na kuokota dhahabu alafu kuitupa ukiwa na akili zako timamu, waccha niende. Nitamdanganya bosi,” aliwaza Dula huku akitafuta kijana mwenye bodaboda ili aweze kumfikisha aliko Aminata.



    Dula alichukua usafiri wa bodaboda hadi alipokuwa Aminata. Kutoka eneo la Kambi ya Fisi hadi Café la Azziz haikumchukua zaidi ya nusu saa. Alimkuta Aminata akimsubiri.



    “Dula nikuombe kitu,” Aminata alimwambia Dula mara baada tu ya Dula kushuka katuika bodaboda.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Nini tena bibie?” alihoji Dula.



    “Samahani lakini, sipendi harufu ya sigara.”



    “Aaah, hilo tu bibie? ok nikiwa na wewe sitovuta hadi niondoke.”



    “Ntashukuru sana.”



    “Vipi bibie, za tokea jana?”



    “Nzuri tu Dula.”



    Dula alikuwa akimwangalia sana Aminata ambaye alikuwa akiendelea kunywa soda yake taratibu. Aliupenda uzuri wake. Alijiona mwenye bahati hasa baada ya kumwona Aminata akiomba msaada na kutaka kuwa marafiki. Hakujua lengo hasa la Aminata hadi kufanya hivyo.



    Aminata aliutumia mwanya huo kuwajua vizuri. Alifurahia ushirikiano na Dula. Kila alipomhitaji Dula alikuwa akifika mara moja. Wakati mwingine alimfuata yeye ili Dula asijue lengo lake. Hata baadhi ya rafiki wa Dula walianza kumjua Aminata.



    Wakiwa katika ukumbi wa starehe wa Triple A. Aminata alitaka kujaribu bahati yake kwa kumuuliza mengi kuhusiana na kundi lao. Kwa kipindi kifupi cha kujuana na Dula aliweza kuonana na wengi katika kikundi hicho akiwemo Mosses ambaye baada ya Dula kumtambulisha alionekana kumtamani sana Aminata.



    “Unakaribisha sana shemeji. Wakati wowote.” Alisema Mosses kisha kutoka baada ya kumsalimia Aminata.



    Aminata alimwangalia sana. Mosses alikuwa ni mrefu mweupe. Sura yake ilikuwa ikifanana na chotara wa Kiarabu. Ni Mnyamwezi wa Tabora lakini maisha yake alikulia Arusha. Alifanikiwa kusoma hadi kidato cha sita. Ni biashara za magendo ndizo zilizomfanya Mosses asiendelee na chuo kwa ni alifaulu vizuri lakini pesa ilimfanya asitamani tena kusoma. Na huo ndio ukawa mwisho wa kurejea yaliyo vitabuni.



    Alianzisha kampuni ya magendo ambayo haikusajiliwa ya kununua magari na kuyauza. Baada ya miaka sita iligundulika lakini hawakuweza kumkamata kwani alikimbilia nchini Kenya na kuishi kwa miaka miwili. Baadaye Mosses alirudi na kuanza ujambazi. Ngome yake aliiweka katika msitu mmoja wa Kambi ya Fisi. Huko hakuweza kuonwa na yeyote kwani alijiimarisha kwa kuweka uzio na walinzi wa kutosha. Alianza kufanya ujambazi na utekaji wa magari akishirikiana na watu wake.





    *****

    Aminata alifanikiwa kujua juu ya Mosses. Sasa roho yake ilitulia. Hakujali kuhusiana na kifo cha Dula ambaye baada ya kubainika ametoa siri za kundi.. Mosses alimpiga risasi na kufa. Aminata baada ya kusikia habari hizo aliamua kujificha kwa muda.



    Alikimbilia jijini Dar es Salaam ambako aliamua kusomea masuala ya Upelelezi na jeshi. Alijua Dula hakumdanganya baada ya kumweluezea ukweli ya siku walivyoteka gari la mzee Peter na familia yake na kuwaua kisha kuchukua mali.



    Aminata alitumia mbinu kubwa sana kumshawishi Dula ili amwelezee. Ni pale alipoamua kumvulia nguo akimaanisha kwamba ni wapenzi. Hapo sasa Dula alidiriki kuunyanyua mdomo wake na kumwambia Aminata kila kitu.



    Usiku huo Dula alijua ungekuwa mrahisi sana. Baada ya kumwambia Aminata juu ya siri za kundi lake. Aminata alimtamkia Dula kuwa anampenda sana na kumwahidi kuwa wake. Dula alifurahi sana. Alimkumbatia Aminata kwa nguvu na kumbusu. Hapo ilikuwa ni kazi rahisi. Dula alijiandikia ushindi kwa mtoto mzuri Aminata.



    “Mbona sikuelewi tena Aminata,” Dula alihoji baada ya kumwona Aminata akitoka kitandani na kukaa kitako katika moja ya masofa yaliyokuwa katika chumba cha hoteli waliyofikia.



    “Hapana Dula, usijali. Siko tayari leo. Nimeumwa sana leo.”



    “Kwa hiyo tutalala tu hivi hivi?”



    “Siyo hivyo. Ni kwa leo tu. Wewe ni mpenzi wangu. Siku yoyote utanitumia uwezavyo.”



    Dula alikubali kwa shingo upande na kulala.





    *****

    Aminata alifanikiwa kumaliza mafunzo yake ya upelelezi. Alirudi Arusha na kujiunga moja kwa moja na Jeshi la Polisi. Ni ujanja wake na uchapaji kazi wake ndio ulipelekea kutunikiwa cheo cha Ofisa Upelelezi. Ilikuwa ni furaha kwake.



    Kati ya mambo ambayo aliyafanya ni uchunguzi na kugundua biashara ya dawa za kulevya iliyomhusisha kigogo mmoja mkubwa serikalini.



    Ni katika mpaka wa Tanzania na Kenya. Eneo liitwalo Namanga ndipo tukio hilo lilipotokea. Akiwa kati ya maafisa wapelelezi wadogo na walioibukia katika kazi hiyo. Aminata aliiamrisha kushushkwa moja ya mabegi ambalo ndani lilikuwa limesheheni nguo.

    Aliliangalia lile begi na hasa baada ya ofisa mmoja mkaguzi kuliwekea alama kumaanisha kwamba lilikuwa safi na kwamba hakukuwa na chochote kibaya. Ofisa huyo alizima alamu ya mashine ya kukagulia na kuipitisha juu ya begi hilo. Baada ya kumaliza aliiwasha. Aminata alikuwa ameona tukio hilo.



    “Nasema shusha tena hilo begi. Sijaridhika na ukaguzi wake.” ofisa yule aliogopa kidogo na kumjia juu Aminata.



    “Nimelikagua, halina shida. Haya mzigo mwingine.” yule ofisa aliamrisha baada ya lile begi kupakiwa kwenye gari.



    “Nimesema, fungua begi,” Aminata alitoa tena amri ambayo safari hii yule ofisa aliitii na kufungua begi. Aminata alitumia kifaa maalumu na kugundua ndani ya lile begi kulikuwa na dawa za kulevya.



    Haraka alichukua simu yake ya upepo na kuwasiliana na polisi ambao walifika maramoja na kuwachukua wale wahusika ambao walikuwa wamewekwa chini ya ulinzi mkali.



    Walipelekwa Kituo cha Polisi cha Kati cha mjini Arusha kwa ajili ya mahojiano huku uchunguzi ukiendelea kuhusiana na biashara hiyo. Watuhumiwa baada ya uchunguzi walifikishwa mahakamani akiwemo kigogo wa serikalini ambaye ndiye aliyewatumia watuhumiwa wenzake kuziingiza dawa hizo zilizotokea nje ya nchi.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wakati wa sherehe moja kubwa ambayo iliwahusu maofisa wapelelezi. Aminata alipata bahati ya kupandishwa cheo na kuwa Ofisa mkuu. Baadaye alihamishiwa jijini Dar es Salaam. Alishindwa kupinga kwani mkuu wa polisi alitaka iwe hivyo. Aminata alihamia Dar es Salaam.



    Huko Dar es Salaam, palikuwa hapakaliki. Mara nyingi alirudi Arusha kwa ajili ya kazi yake moja tu. Kazi ya kuuangamiza mtandao wa Mosses Ndula. Ulikuwa ni mtafutano baina yake na Mosses Ndula ambaye alidhamiria kumweka Aminata mikononi mwake.





    *****

    John alikuwa hana raha. Alimfikiria sana wakati huo. Alikumbuka kwamba hakumwachia namba za simu Aminata bali alimwambia tu amtafute baada ya mazishi ya ndugu zake.



    Alifikiria sana atampataje na mwisho aliamua arudi kituo cha polisi kwani mara ya kwanza kufika kituoni hapo alikuwa amefungwa pingu huku Aminata akiwa ni moja ya watu waliompeleka kituoni hapo kutokana na kesi yake kuwa kubwa japo iligundulika kuwa si yeye aliyemuua mfanyabiashara anayedaiwa kuuliwa. Aliingia na kumkuta Afande Nicco na kumsalimia.



    “Habari yako afande.”



    “Ahh! We mwalifu, umerudi tena, umejileta eeh?” Afande Nicco aliongea kwa mzaha uliosababisha John acheke.



    “Karibu tena, leo umekuja kumshtaki mtu au kunisalimia tu?” Aliendelea na utani afande Nicco.



    "Hapana nimekuja kukusalimia na kuulizia jambo moja. Kuna dada mmoja alikuwa pamoja na Afande Mushi waliponileta siku ya kwanza. Anaitwa Aminata.”



    "Aminata, we unataka kutembea na ofisa upelelezi?” Alisema Afande Nicco kwa mshangao na kauli zake za utani. John alicheka kidogo.



    "Hapana, kuna jambo anataka nizungumze naye, aliniambia nimtafute."



    “Kwani huna namba zake za simu?”



    “Hapana, hakunipa siku hiyo. Kama unayo naomba unisaidie.”



    "Sawa mi n’takupa namba zake za simu na kwa nini hakukuachia namba zake?" Alihoji Afande Nicco.



    "Sielewi, ila alisema tu nimtafute." Afande Nicco alimpa John namba za simu kisha waliagana. John aliwasha gari lake na kuelekea nyumbani. Alichukua zile namba na kumpigia Aminata.



    "Haloo!"



    "Habari yako, sijui nani mwenzangu?" Sauti ya upande wa pili ilikuwa ni ya Aminata ambaye alitaka kujua ni nani aliyempigia simu.



    "John, mtoto wa Amigolas, marehemu sasa, tulikutana Hospitali ya Mount Meru na kunitaka n’kutafute baada ya mazishi ya ndugu zangu."



    "Ooh! John, pole sana. Ila umechelewa sana kunitafuta. Mimi nipo hapa McDonald's Pub kama utaweza kufika hapa muda huu itakuwa vizuri zaidi." Aminata aliongea kwa furaha baada ya kujua aliyempigia simu ni John.



    "Nakuja hapo sasa hivi Aminata."



    "Sawa nakusubiri John.”



    Aminata alikumbuka dhamira yake. alijua akiwa na John mpango wake utafanikiwa kwa asilimia mia moja. Alijua pigo alilolipata yeye ni sawa na alilolipata John na hivyo ingekuwa rahisi sana kufanya kazi pamoja.



    Alikuwa tayari ameshaijua vyema familia yote ya mzee Amigolas. Aliijua baada ya kutaka kuwa katika upelelezi wa wauaji wa familia hiyo.



    Japokuwa alishafahamu mtandao mzima lakini Aminata hakudiriki kuwaeleza polisi juu ya mtandao huo kwani lengo lake lilikuwa ni moja tu. Kulisambaratisha.



    ******

    John aliwasha gari lake . Askari wa mlangoni aliwahi kufungua geti na John kuondoa gari kwa kasi ili amuwahi Aminata. Ilimchukua dakika 10 mpaka kufika McDonald's Pub. Alikuta magari mengi nje. Alilipaki gari lake karibu na mlango wa kuingilia ndani. Aliteremka na kutoa simu yake na kumpigia Aminata.



    "Haloo Aminata."



    "John, njoo moja kwa moja hadi counter, nipo peke yangu hapa."



    "Sawa Aminata, nakuja hapo sasa hivi," John alielekea hadi counter na kumkuta Aminata akiwa ameshikilia glasi ya wine. Mhudumu alipomwona John alimkaribisha.



    “Karibu kaka, n’kusaidie nini?”



    "Hapana sitatumia chochote.”



    “John, you should take something... mhudumu, mletee wine kama yangu,” Aminata alimwagizia John wine. Walikaa na kuanza kuongea baada ya wine kuletwa.



    “John,” aliita Aminata.



    “Yes Aminata, nakusikiliza.”



    “Pole sana na msiba wa wazazi wako na ndugu zako. Nauhakika polisi bado wanaendelea na uchunguzi. Mimi ni ofisa upelelezi ndiyo maana uliniona siku ambayo ulikamatwa niliongozana pamoja na Inspekta Morris na Afande Mushi.



    Wote kwa sasa wanafanya uchunguzi wa nani anahusika na vifo vya wazazi wako na ndugu zako.”



    “Natamani sana kuwajua watu hao,” alisema John huku kainamisha kichwa chini na kusababisha huruma kwa Aminata.



    “Utawajua John, kabla hawajakamatwa, mimi na wewe tutawakamata."



    “Tutawakamata vipi lakini?” Alihoji John kwa mshangao kwani hakuwa na uzoefu wa kukamata wahalifu. Iweje apewe jukumu hilo.



    “Mi siyo polisi, n’tawezaje Aminata.”



    “Namaanisha, nataka ulipe kisasi na si kuwakamata. Kama walivyoua ndugu zako, yapasa na wao waangamizwe. We ni mwanamume. Amka. Wale wakikamatwa na polisi baadaye watatoka. Inatakiwa wamalizwe kabisa.”



    “Kumbe unawajua Aminata?” Alihoji John.



    “Ndiyo John, ni mtandao mkubwa sana wa kihalifu, unaoogopeka sana. Kiongozi wao anaitwa Mosses Ndula, huwa hakai hapa nchini, anakuja bila yeyote kujua nakuondoka. Na huyo ndiye jabali lao. Ndiye aliyewatuma watu wake wawaue wazazi na ndugu zako. Inawezekana pia wakawa wanawatafuta na nyie wawili.”



    “Sisi wawili, mi na nani?”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Unamfahamu pacha wangu, unamfahamu Antony?”



    "Ndiyo John, kwenu nawafahamu japo nyie hamnifahamu. N’mefanya kazi nyingi sana kumsaidia baba yako. Na hiyo ilinifanya niwajue..... Nadhani ni muda wa kwenda. Nitakuelezea mengi tukifika kwangu."



    "Naomba tuongozane, twende pamoja nyumbani kwetu ukapafahamu," John alimwambia Aminata ili waongozane kwenda kwao.



    "Sawa John," Aminata alikubali na kuongozana na John. Hakutumia usafiri wake. Aliliacha na kuondoka pamoja na John aliyekuwa na usafiri wake.





    *****

    Walitumia dakika ishirini tu kufika Njiro nyumbani kwa kina John. Walikuta watu watatu wakiwa wamesimama nje ya geti. Mlinzi aliwafungulia na kuingia. John alikuwa bado hajawatambua hadi alipofikia geti kabisa. Mlinzi alifungua geti kubwa na kuliruhusu gari la John kuingia. John sasa alimtambua mmoja kati ya wale wageni.



    "Hawa ni wachimbaji wa mgodi wa baba,” John alimwelezea Aminata.



    "Namkumbuka mmoja tu, aliyevaa kapelo. Sijui wanataka nini.” John alishuka kwenye gari na kumfungulia Aminata mlango, alimkaribisha kisha kuwafuata wale wachimbaji.



    "Mbago bila shaka," John aliuliza.



    "Ndiyo mkuu, ni mimi, habari za siku nyingi bosi?" Antony naye alikuwa akitoka nje baada ya kusikia gari likiingia na watu wakiongea. Alisimama mlangoni. Aminata alimwangalia sana kisha kumgeukia John. Hakuona tofauti kati yao. Walikuwa wamefanana sana.



    "Salama tu, habari za Mererani bwana Mbago." Aliwasalimia na wachimbaji wengine walioongozana na Mbago.



    "Kule hali siyo nzuri kabisa bosi."



    "Kwa nini sio nzuri?” Alihoji John.



    "Hatuelewi hatma yetu kwani mgodi umeuzwa bila ya kupewa taarifa. Ndio tumechukua uamuzi wa kuja kujua moja ikiwamo kuhoji imekuaje kimyakimya." Alielezea Mbago kwa masikitiko huku wenzake wakiitikia kwa kichwa kuashiria anachosema ni kweli.



    "Mgodi umeuzwa?” John na Antony kwa pamoja walitahamaki. Haraka Antony aliingia ndani na kutoka na hati ya umiliki wa mgodi inayoonyesha mmiliki halali wa mgodi ni baba yao Amigolasi.



    John aliangaliana na Aminata kwa muda. Hakujua amwambie nini hadi pale Antony alipotoka nje na karatasi iliyoonyesha hati ya umiliki wa mgodi.



    "Haiwezekani, hati hii hapa,” Antony aliwaonyesha. “Hii si ndo hati ya mzee? John embu itazame mwenyewe. Ni nani huyo anayeleta mchezo?” Antony alimkabidhi ile hati John ambaye aliiangalia kisha nay eye kumpa Aminata aiangalie.



    "Nani kaja kuwapa hizo taarifa? Alihoji John huku akimwangalia Aminata kana kwamba Aminata alijua kinachoendelea. Aminata alikuwa kimya akisikiliza malalamiko na utetezi wa pande zote mbili. Wachimbaji na mabosi wao. Mbago aliwaelezea namna ilivyokuwa hadi wakaamua kuwafukuza kwa mawe na kisha kuitisha kikao cha kujadili safari ya kuja kuonana na wao.



    "Mmefanya vizuri sana. nashukuru sana kwa hizo taarifa. Kuna watu wanataka kutudhulumu haki yetu. Labda sio mimi.” John alisema kwa ukweli huku akimrudishia Antony ile hati ili aipeleke ndani.



    “Tutalishughulikia hilo, ila waambie wenzako kwamba mgodi haujauzwa, kazi ipo na mambo yakitulia m’taendelea kama kawaida." Antony alihitimisha ili kuwaruhusu Mbago na wenzake wawawahi kuwajulisha wenzao.



    "Tunashukuru sana bosi. Siye tunaenda. Mbaki salama." Mbago na wenzake waliondoka baada ya kupata jibu. Hawakujua kwamba wamewaachia John na Antony kazi kubwa sana. John alionekana kuchanganyikiwa.





    ****

    Ni aminata peke yake ndiye aliyeweza kumliwaza John. Aliamua kuwa naye karibu zaidi ili aweze kumtoa katika hali ile. Si kwa hilo tu bali pia Aminata alikuwa anaonyesha kila dalili za kumpenda John kimapenzi. Ni kwa kipindi kirefu sana amekuwa kattika hali hiyo ya upweke kwa ajili ya kazi.



    Aminata alikuwa ameshapajua nyumbani kwa kina John na hivyo alifika mara kwa mara ili kuendeleza mipango yao.



    Aminata alipata nafasi ya kuongea usiku huo. Hakwenda nyumbani kwake bali aliamua kulala nyumbani kwa kina John kwa ajili ya kuongea mengi. Aminata alimsimulia John yote yaliyomtokea hadi akaamua kuwa mpelelezi.



    “Niliamua nikajiapiza kwamba sitawasamehe nan i lazima niwakamate na niwaangamize mimi mwenyewe. Baada ya kukufatilia na kujua wewe ni mtoto wa mzee Amigolas, na bada ya kuona pigo nililolipata mimi na wewe umelipata pamoja na pacha wako. Na pia John wewe unaonekana si lele mama. Wewe na Pacha mnaonekana mmeshiba sana. ni watu wenye nguvu za kupambana. Hivyo kwa mafunzo niliyoyapata tukichanganya na ninavyowaona nyie. Tutawamaliza hata kama wako wengi vipi.” Aminata alimwambia John huku akicheka kwa lengo la kumshawishi wawe pamoja.



    John alisimama. Alijiona kama mshindi na asiyeogopa hatari yoyote. Alikumbuka wazazi wake na ndugu zake walivyouliwa. Aliwakumbuka Mbago pamoja na wenzake waliokuja siku chache zilizopita kuwaeleza juu ya migodi. Yeye kama mwanamume iweje akae nyuma wakati Aminata amejitoa kupambana dhidi ya dhulma.



    “Tuko pamoja Aminata lazima tuwaangamize. Kesho asubuhi nitaongea na Antony tujue tunaanza lini kazi. Hata kama wameshajimilikisha mgodi lazima tuurudishe. Hizo ni dhuluma. Hatuwezi kuziacha zikatufilisi sisi. Walishachukua roho za ndugu zangu. Sasa wachukue na yakwangu nay a Antony kama wanaweza.” John alisema kwa hasira kali.



    Aminata alimfuata na kumshika kisha kumkalisha juu ya kitanda. Pamoja na baridi kali ya mjini Arusha, John alitokwa na jasho kali. Joto lilisababishwa na hasira. Hapo Aminata alimwelewa John kwamba yu tayari kwa mapambano.



    “John,” aliita Aminata.... “Wewe ni mwanamume unayeonekana shupavu. Ni mwanamume unayeweza kupambana na pia unamvutia sana mwanamke. Mvuto wako siwezi kuuvumilia pamoja na kwamba unayo hasira. Leo nipo kwako. Sitalala peke angu. Najua Antony ameshalala. Niazime mwili wako kwa usiku huu wa hii baridi,” Aminata alishindwa kuvumilia kila alipomwangalia John ambaye alikuwa amevua shati na kubakiwa na kaushi iliyombana vizuri na kufanya misuli yake itoke nje.



    Aminata alipata nafasi ya kuushika mwili wa John kila alipokuwa akimbembeleza. Hapo alijihisi kumvamia John japokuwa alikuwa na hasira. Alijaribu umtuliza mpaka alipoweza kumwambia alichokitaka.



    John aliyasikia aliyoyasemaAminata. Hakuonyeshwa kushangaa kusikia maneno yale. Hakuwa na kufanya zaidi ya kunyinyakulia ushindi murua wa mezani baada ya mpinzani wake kuweka mikono chini kuashiria hawezi kushindana.



    Ukawa ni mgeuzano wa kila aina katika mbao za futi sita kila upande. Godoro la kisasa zaidi ya lilivyotumika kabla lilionja joto ya migusano na vilio vya mahaba kutoka kwa ofisa mpelelezi Aminata.



    Tukio liliendelea tena na tena. Ukawa ni usiku wa bashasha uliolakiwa vizuri na miili iliyokuwa tayari kujifunga na kuwa pamoja. John alisahau hasira zake na kudhulumiwa kwa mgodi. Aminata naye akasahau kazi yake ya ofisa upelelezi. Mtifuano mkali ulimalizika pakiwa panaelekea kupambazuka. Wote walifurahia mchezo huo

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Asubuhi John alimfata Antony. Alimwelza juu ya kila alichoambiwa na Aminata. Antony hakuwa na pingamizi kwani alijua hakuna njia nyingine endapo wahusika walishajimilikisha mgodi. Hivyo alijiunga nao ili kuhakikisha wanafanikiwa.



    John alimwita Aminata na kumweleza juu ya Antony kukubali. Aminata alifurahi sana. alimwangalia Antony vizuri kwa lengo la kuwatofautisha pindi watakapokutana. Antony ambaye ndiye aliyekuwa mdogo, alikuwa mweupe kidogo kuliko John. Pia Antony alikuwa ni mpole kwa zaidi ya John.



    “Mmefanana sana nyie watu. Antony ni mweupe hapo ndo sitawachangamya.” Antony aliangaliana na John kisha wakacheka.



    “Acha utania wako Aminata,” John alisema huku akimshika mkono Aminata na kumtambulisha vizuri Antony.



    “Huyu anaitwa Aminata. Ni shemeji yako.”



    “Nilishaelewa mapema, nilikuwa nasubiri tu nisikie kauli yako. Hongera kaka.”



    “Asante.” Hapohapo Aminata nay eye akaongea kuwaambia John na Antony juu ya mpango wake.



    “Nataka kwanza mjue kitu gani tutaanza nacho. Kazi ni kubwa sana kuliko huku kutambulishana. Inahitajika mfanye mazoezi hasa ya kulenga shabaha. John we ulikutwa na bastola lakini sidhani kama unajua kuitumia vizuri.”



    “Najua sana, sema nakusikiliza.”



    “Mmmh. Na mbona wale majambazi walikimbia hukuitumia wakati yule mfanyabiashara alivyovamiwa benki? Au hukujua kama uko nayo?” John na Antony walicheka sana kisha wakasema kwa pamoja.



    “Basi tufundishe ofisa.”



    Zoezi likaanza mara moja. Aminata aliwapeleka sehemu maalumu wa ajili ya kuwafundisha nyumbani kwake Sakina.



    Jambo la kwanza alilofanya Aminata ni kuwafundisha mbinu mbalimbali za kutumia. Aliwafundisha kutumia silaha kwa kulenga shabaha pamoja na namna ya kuwa makini wakati unapokabiliana na adui yako anayekuhisi unamchunguza. Baada ya muda wote walijua.



    AMINATA ANAFANIKIWA KUWASHAWISHI JOHN NA ANTONY KUJIUNGA NAYE KWA AJILI YA KUANGAMIZA KUNDI LA MOSSES NDULA. ANAWAPA MAFUNZO AMBAYO ALISHAYAPATA AKIWA KATIKA MAFUNZO YA JESHI.



    JE WATAFANIKIWA KATIKA MPANGO WAO WALIOUDHAMIRIA…..



    USIKOSE SEHEMU YA SIMULIZI HI

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    ITAENDELEA



0 comments:

Post a Comment

Blog