Search This Blog

Sunday 22 May 2022

HII NI DUNIA AU KUZIMU? - 3

 







    Simulizi : Hii Ni Dunia Au Kuzimu?

    Sehemu Ya Tatu (3)

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    "Amepata mshtuko wa ghafla ni kama mtu aliyeona kitu cha kutisha sana kwani hata moyo wake ulipunguza kasi ya mapigo kwa kiasi kikubwa,......tukiangalia hata uangukaji wake si ule mshtuko wa kawaida wa mtu aliyekumbwa na jambo la kawaida...hebu tazameni kupitia hii video iliyorekodiwa na kamera ya ulinzi wakati wa tukio." alipoweka kituo hapo akaiwasha kompyuta iliyoko mbele kabisa kwa kutumia rimoti. Wote wakageuka kuitazama kompyuta hiyo. Picha ilionekana kuanzia pale ambapo Tereza akiwa anamtazama Baba yake akiwa anatetemeka lakini hapohapo akageuka kushoto ghafla sana akatoa macho kwa hofu kubwa halafu kukatokea kitu cha ajabu kuhusu uangukaji wake, Tereza alikuwa kama aliyesukumwa kwani alirudishwa nyuma kidogo na kuanguka kwa kishindo kikubwa sana.



    "hebu rudisha nyuma kidogo....enhe! Hapo hapo, acha" aliagiza Bencov kisha kuanza tena kuangalia kwa umakini zaidi.



    "hii video inanichanganya, kilichomuangusha huyu binti nini?" akauliza Bencov baada ya ile video kufika mwisho. Wote wakahema kwa nguvu na kutazamana usoni. Alipoona kimya kimetanda akarudia tena.



    "Backa alikuwa mbele ya huyu binti lakini kilichofanya ageuke ni nini sasa?" hapa Merina akasimama na kusema.



    "hakuna kitu kingine kilichomuangusha Tereza Bencov, huyu binti ameanguka na kupoteza fahamu baada ya baba yake kuwa katika hali mbaya na ya kutisha....!"



    "umeiona video vizuri?" akauliza Bencov, hakuwa na raha tena aliona kama kazi yake aliyoipanga inakwenda kumuwiya ugumu.



    "nimeiona" alijibu Merina kisha akaendelea.



    "Backa alikuwa mbele lakini kama utaiangalia hiyo video vizuri utagundua kuwa hakuna kilichomuangusha kingine zaidi ya hofu juu ya baba yake, kivipi? Baba yake alikuwa mbele kama nilivyosema awali lakini Dr. Cartley alikuwa amesimama upande wa kushoto kwa maana hiyo basi, wakati Backa amekumbwa na yale maumivu ya kusababisha kutoka mishipa mwili mzima, Dr. Kuna kitu aliongea kwa msisitizo juu ya hali ya Backa na hilo ndilo lililomfanya Tereza kudondoka na kupoteza fahamu" alimaliza kuongea Tereza lakini bado Bencov akawa mgumu kuamini kama hilo ndilo lililopelekea binti huyo kudondoka.



    "tunaomba sauti iliyorekodiwa pale" aliagiza Merina ili kumuweka kila mtu sawa mahali pale. kadi lida ikaletwa na kuchomekwa kwenye kompyuta kisha kuruhusu sauti iliyokuwa sambamba na picha. Kila kitu kikaoneshwa kama ambavyo alieleza Merina, hapo mjadala ukafa na kila mmoja akaamini, sasa likawa ni jambo moja tu la kuwa binti huyo atapona vipi na kwa muda gani ili aweze kuanza kazi yao. Wakajadili vya kutosha kisha Dr. Henry akasema kuwa aachiwe hiyo kazi kwa muda wa wiki moja kila kitu kitakuwa sawa. Mjadala ukafa kila mmoja akarudi mahali pake pa kazi. Merina alipotoka pale moja kwa moja alierejea kwenye chumba chake, huko alikuwa akitafakari mengi sana lakini kubwa na lililokuwa likimuumiza kichwa ni lile la kumuangusha merina chini kisha kupoteza fahamu. Aliwaza sana lakini jibu alilokosa abadan ni nani au ni kitu gani kilichomfanya adondoke, kwanza ni ghafla sana kutokea. Aliwaza na kujiuliza lakini jibu hakulipata kabisa mwisho akakata shauri kwenda moja kwa moja kwa Bosi wake ili wakajaribu kulijadili hilo jambo kwa pamoja kwani hali walishaanza kuiona ngumu.



    "Afadhali ulivyokuja my Lady Devil, ni nini kile? Inabidi nikuulize kabl ya kukupa pongezi" aliongea Dr. Lee. Merina akajaribu kufikiri kwa muda kama anaweza kulijibu swali la bosi wake lakini akaishia kugumia tu Mg! Mara baada ya kugundua kumbe hata yeye alijiuliza na hakupata jibu hivyo kuja hapo ilikuwa ni huwenda labda yeye anajua.



    "ndiyo maana nimekuja kwako Boss" alijibu Merina akiwa anamtazama Dr. Lee usoni ili aweze kumuona atakavyoipokea kauli yake hiyo. Dr. Lee akahema kama Cobla kisha akatulia kwa muda mrefu sana.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Umejitahidi kuwazugisha pale, nikupongeze kwa hilo lakini kwa ibada zetu juu ya wale wanaonifanya niko hai hadi sasa" akatulia kidogo Dr. Lee na kumtazama Tereza usoni. kabla ya kumalizia.



    "kuna kiumbe kinalengo la kuharibu mpango wetu na sisi tumeingia kwenye njia siyo Merina nahofia huwenda tukaangamia wote tusipokuwa makini"



    "ni kiumbe gani sasa Boss ambacho kinapingana na sisi?" akauliza Merina.



    "Hata mimi najiuliza hivyo hivyo Merina huwenda huyu si yule aliyenipa uhai mimi, huyu siye kabisa" alijibu kinyonge sana Dr. Lee, alikuwa akiiona hatari ya kuishi hivyo milele bila kupata tiba ya mwisho aliyowahi kuahidiwa kipindi cha miaka miwili nyuma. Hakuamini kama kweli angeweza kuishi kama binadamu aliye hai katika maisha yake hapo alikuwa alijiona si mwanadamu aliyekamilika hata kidogo na alikuwa akihitaji kuja kusimama na kuwa mkuu wa dunia yote kwa kuanzisha dini yake na maisha mapya kwa kila kiumbe kitakachoishi duniani lakini ikiwa ni kwa mataifa machache sana huku mataifa mengi ya ki-Afrika yakiwa yameangamia kwa mikono yake. Merina alichoka kabisa kabisa nani angelikuwa malikia kama si yeye, yeye ndiye angelikuja kuwa malikia wa dunia huku Dr. Lee akiwa ndiye kinara. Alijikuta amekaa mbele ya Dr. Lee bila kupenda lakini Dr. Lee akamwambia Merina kuwa kwa muda huo hakuna budi kumfuata King Bondo katika msitu mkubwa wa kijani uliopo pembezoni mwa kisiwa hicho cha Madagascar.



    "Tunazo siku sita pekee za kusubiri kwenda huko. Kama Tereza akiwahi kuamka kitandani kwa muda huo ambao Dr. Henry ameahidi basi safari ya kwenda huko msituni itakufa lakini asipoamka kwa siku hizo tano basi ni lazima tukaombe msaada wa King Bondo.



    Upepo mkali ulikuwa ukivuma, anga lilikuwa ni la giza kidogo huku kukiwa na dalili za mvua. Hali hiyo iliashiria kama ingeendelea basi mvua ingekunya muda wowote ule. Upepo ule ulikuwa ni mkali kiasi kwamba madirisha ya jumba kubwa lililopo Katikati ya msitu yalikuwa yakipiga kwa kujifunga na kujifungua yenyewe. Hali ile ilizalisha kelele ambayo hata kama ungekuwa umetopea kwenye usingizi wa fofofo, usingeliweza kuhimili kelele zile. Ndani ya chumba kimoja kulisikika ala ya muziki laini sana ambayo ni wazi ilikuwa ikitoka kama si kwenye kinanda basi ni piano moja maridadi sana. Ala hiyo ya muziki, haikujulikana ni ya muziki kutokea Taifa gani lakini ilikuwa ni nzuri na yenye kumfanya mtu aweze kupitiwa na usingizi mnono mno. Lakini zile kelele za kupiga kwa dirisha hazikukoma kabisa na zilizidi kuleta kero kubwa sana. Ndani ya kile chumba hakukuwa pweke bali kulionekana binti mrembo sana akiwa kwenye shela la harusi safi akiwa amelala kwenye kitanda cha gharama kubwa. Kelele zile zilionekena kumpa kero sana kwani kila mara alikuwa akijigeuza pale kitandani bila kunyanyuka. Upepo nje ukazidi, madirisha yakaongeza kasi ya kujipigiza hadi kufanya baadhi ya vioo vya madirisha ya vyumba kadhaa kuanza kuvunjika. Giza lilikuwa zito sana. Ni chumba kile pekee ndiyo vioo vyake havikuweza kuvunjika lakini vilikuwa vikijipiga kwa nguvu sana. Yule binti mrembo pale kitandani aliyekuwa amepambwa na vazi la shela akanyanyuka na kukaa kitako lakini





    hakuwa amefumbua macho yake. Mungu wangu! Huyu msichana alikuwa amefungwa Bandeji kubwa sana kichwani mwake kiasi cha kubakishwa sehemu ya macho pekee. Alikuwa ni Tereza,....Tereza?" Ndiyo, alikuwa ni Tereza akiwa ndani ya Shela la gharama kubwa mno lenye rangi nyeupe kabisa. Huyu binti si yuko mahututi tena zikiwa zimepita siku tatu bila kufumbua macho wala kurudiwa na fahamu? sasa kwanini huku kwenye hili jumba la kutisha tena lililokuwa katikati ya msitu? Amefikaje huku? Na kwanini awe huku? Je, kule kitandani ni nani amelala? Inatisha.



    Madirisha yale hakutaka yaendelee kuwa kero kwake kwani alionekana kuhitaji kupumzika zaidi na siyo kupigiwa kelele na vitu ambavyo haviongei. Alijinyanyua pale kitandani alipokuwa amekaa kitako kisha kupiga hatua ndogo ndogo hadi dirishani lakini akiwa ameyafumba macho yake vilevile hakuhitaji kuyafumbua hata kidogo, haikujulikana kwanini. Pamoja kuwa alikuwa amefumba macho lakini aliweza kulifuata kila dirisha la mule chumbani mwake na kufanikiwa kuyafunga yote, kimya kikatanda mule ndani. Ala ya muziki ule laini ikaanza kutoweka taratibu, ilitoweka ikatoweka, ikatoweka kabisa na kubaki kimyaaa! Tereza wa maajabu akaanza kusogea kwenye kile kitanda kwa mwendo uleule wa kiharusi hadi alipokifikia akakaa.



    "My Queeen!.....my Queeeeen......my Queeeeeeeeen!" sauti nzito ilivuma mule ndani ya lile jumba na ilisikika kutokea mbali sana kutokana na sauti hiyo msikiko wake. Ilijirudia zaidi ya mara nyingi hiyo sauti na kwa jinsi ilivyokuwa ikijirudia ndivyo ilivyokuwa ikizidi kusikika kwa nguvu na hatimaye ikaonekana sasa muitaji wa sauti hiyo hakuwa mbali ya chumba hicho lakini mwangwi ule haukukoma hata kidogo. Tereza wa ajabu alinyanyua kichwa chake juu kwa haraka sana huku akiwa bado amefumba macho kisha akaachia tabasamu pana. Alionekana kuna kuimbe alikuwa akimpokea chumbani hapo kwa kunyoosha mikono yake mbele japo kiumbe hicho hakikuonekana kwa macho ya kawaida kisha kulala chali giza likatanda, sauti za milio ya mahaba zikakimeza kile chumba.



    KWENYE HIMAYA YA DR. LEE.



    Hali ya Tereza ilizidi kuwa mbaya tena mbaya zaidi, kwani hakuonesha hata ile hali ya kupumua, kitu hicho kikawa ni hofu kubwa kwa Dr. Henry. Hakuamini kama ahadi aliyowaahidi mabosi zake ingeweza kutimia.



    "ni siku ya nne sasa Dokta lakini hakuna matumaini ya huyu binti kunyanyuka, hivi unadhani mabosi watatuelewa kweli endapo huyu binti akishindwa kunyanyuka hapa?" lilikuwa ni swali kutoka kwa dokta msaidizi wa Henry.



    "huwezi amini jinsi ninavyochanganyikiwa, kwanini lakini huyu mwanamke hataki kunyanyuka" Alisema Dr. Henry kisha akatulia kidogo, akaitoa mawani yake iliyopo machoni na kuiweka mezani kisha akamtazama msaidizi wake. Akasema.



    "unajua kesho mabosi wanataka majibu ya kuamka kwa huyu?"



    "ndiyo najua kiongozi" akajibu yule msaidizi wa Dokta.



    "chukua vipimo tukajue mapigo yake ya moyo jinsi yanavyokwenda, huwenda yakawa yamebadilika unajua naomba sana iwe hivyo" akasema kisha wakachukua vipimo na kuelekea kwenye chumba ambacho amelazwa Tereza akiwa katika hali ya kuto kujitambua kabisa. Tereza huyu alikuwa ni yuleyule wa usiku kule kwenye jumba la kutisha lakini huyu alikuwa ni tofauti na yule kwani huyu alikuwa hajitambui kitandani na yule alikuwa anaweza kufanya kila kitu japo alikuwa hafumbui macho. Pia alikuwa yuko ndani ta shela kubwa na la gharama sana tofauti na huku akiwa ni mwenye nguo zake zilezile alizotekewa nazo. Hiki ni kizungumkuti.



    "Inaonesha mapigo ya moyo yapo chini sana kiongozi hii mbona kama inanichanganya" alisema yule msaidizi wa Daktari Henry.



    "hapana haiwezi kuwa hivyo saa kumi na moja asubuhi nilimpima mapigo ya moyo yalikuwa yanapiga vizuri tu sasa imekuwaje eenh?" aliuliza huku akiwa anamtazama Tereza kwa jinsi alivyokuwa na hali mbaya pale kitandani yaani alikuwa akiomba dua muda wowote binti huyo anyanyuke ili aachane na lawama kutoka kwa mabosi zake.



    "hebu sogea nimpime mwenyewe labda masikio yako hayako sawa" alisema huku akichukua kifaa cha kupia mapigo ya moyo na kukiweka vizuri masikioni mwake lakini kabla ya kufanya chochote, kuna binti alikuja mahali hapo na kumwambia kuwa alikuwa akihitajika chumbani kwa bosi. Dr. Henry aliondoka hapo haraka sana bila kufanya kitu chochote alichokitarajia kukifanya. Alitembea kwa mwendo wa haraka sana hadi kufika huko.



    "vipi maendeleo ya mgonjwa wako maana imesalia siku moja tu?" aliulizwa swali hilo Henry na Dr. Lee. Dr. Henry akajibu kuwa hali ya Tereza bado ni mbaya sana na haijulikani ni muda gani atakuwa sawa. Jibu hilo likawa ni mwiba mkali sana kwa Dr. Lee, alikuwa akitetemeka mithili ya mtoto mdogo mwenye Degedege.



    "kesho ukija na jibu hili Henry jua hili jambia hili" akanyoosha jambia juu kumuelekea daktari kisha akamalizia.



    "litakata kichwa chako. Siweze kukuacha hai hata iweje, huwezi kunidanganya kwamba unaweza kumnyanyua huyo binti kumbe huwezi. Unadhani ni nani mwenye moyo wa kike wa kukufanya wewe uishi kwa amani huku ukiwa umefanya uzembe mkubwa kiasi cha kukera" aliongea Dr. Lee akiwa anatazma pembeni ili kuweza angalau kuzizuia hasira zake.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "na na.....niamini.....!"



    "hakuna cha na na wala nini hapa, nitakwenda kukata kichwa chako kikae tu chumbani kwangu kama pambo kwa kushindwa kumnyanyua huyo binti wewe" alifoka kwa sauti kubwa iliyokuwa ikitokea kooni kisha mzee huyo akalegea na kutulia kimya. Merina akamwambia Dr. Henry atoke humo ndani na ahakikishe Tereza ananyanyuka kinyume na hapo atatafuta Mbeleko ya kumbebea Lee. Dr. Henry akatoka humo ndani akiwa amechanganyikiwa kupita kawaida. Hadi Dr. Lee kutokewa na ile hali ya kupoteza nguvu, ni wazi alikuwa yupo kwenye hasira mbaya sana. Kazi ya kuhakikisha Tereza anakuwa salama ilikuwa mikononi mwake, ni yeye wa kuweza kumrejesha binti huyo katika hali nzuri ya kuishi tena. Mitambo ikaunganishwa na kuanza kuchomekwa kwenye mwili wa huyo binti. Mapigo ya moyo yalikuwa bado yapo chini vivo hivyo na dalili ya kuonesha kuwa hali ya usalama ingetokea, haikuwepo. Hadi giza linaingia hakukuwa na dalili au matokeo mazuri ya kumpa bosi. Walichoka.



    Katikati ya usiku wa saa sita kama ilivyo ada kule kwenye nyumba ya maajabu ambayo haikujulikana chanzo chake wala nini sababu ya kuwa kule. Tereza yule wa ajabu alikuwa amelala fofofo tena. Alikuwa kwenye usingizi mzito sana. Jumba lote hilo lilikuwa limemezwa na giza zito kasoro chumbani mwa Tereza wa ajabu pekee ndiyo kulikwa na mwanga hafifu wa mishumaa miwili iliyokuwa ikiwaka. Upepo ulikuwa ukivuma nje kwa nguvu sana lakini ndani kulikuwa na utulivu mkubwa wa kutisha. Kitu cha ajabu ni kwamba bado alikuwa kwenye mavazi yaleyale ya uharusi hakuwa amebadilisha au yamebadilishwa. Kadiri muda ulivyokuwa ukisonga ndivyo chumba kile kilivyokuwa kikitisha. Kulionekana kiumbe kimoja cha ajabu sana chenye kasi kubwa ambacho kilikuwa kikitokea na kupotea mule ndani na hali hiyo ilikuwa ikitokea kila baada ya sekunde kumi na tano. Nini hii? Ala ya muziki ule usioeleweka ikaanza taratibu, ulianza hivyo hadi ukachanganya kabisa na kufanya hali izidi kutisha maradufu mule ndani, mwanga ukaongezeka baada ya kiumbe kile kilichokuwa kikija na kupotea kuwasha mishumaa mingi zaidi na kuleta hali nzuri mule ndani kisha kiumbe hicho kikatulia katikati ya chumba kile kikiwa kimejiinamia chini. Kilinyanyua shingo taratibu lakini hakikuonekana sura yake japo kwa mavazi yake kilionekana ni cha jinsia ya kike. Swali la kujiuliza, inamaana hiki ndicho kilichofanya mapenzi na Tereza wa ajabu usiku wa giza lililopita? kama jibu ni ndiyo, itawezekana vipi kiumbe chenye jinsia sawa na Tereza kuweza kushiriki mapenzi usiku ule au zile zilikuwa ni sauti tu za mahaba lakini hazikutokea humo ndani na kama jibu ni hapana, ni vipi hiyo hali iliyokuwa inasonga humo ndani. Kiumbe kile kilikuwa kimevaa vazi la shela pia kama Tereza wa ajabu alivyo vaa, juu usoni kulipita kitambaa chepesi sana ambacho si rahisi kuiona kwa uzuri sura halisi ya hicho kiumbe. Ile ala ya muziki kama kawaida ikaenda kuacha kulia tena kisha zile sauti za usiku uliopita zikajirudia lakini leo ikiwa ni tofauti kidogo kwani kila sauti zilivyokuwa zikiongezeka ndivyo harufu ya manukato makali yalivyokuwa yakizidi kunukia.



    "my Queeeeen!.....my Queeeeen........My Queeeeeeeeeeeeeeeeen!!" mwisho sauti kali ikasikika ambayo ilimfanya Tereza wa ajabu kushtuka kutoka usingizini na kukaa kitako ghafla kisha kuanza kutazamana na kile kiumbe huku Tereza huyo akiwa hataki kufumbua macho. Sauti ya my queeen haikukoma ilizidi kuwa kali vibaya sana kiasi kwamba ingeweza kuumiza ngoma za masikio za kiumbe wa kawaida mahali hapo lakini si kwa kile kiumbe cha ajabu wala Tereza wa ajabu aliyeonekana kudhurika na ile sauti.



    "My Quuueeeeeeeeeen!" sauti kali kabisa ilisikika, hii iliambatana na kelele nyingine za sauti ya kike iliyokuwa kama ikiumia. Ilikuwa ni ya kike hiyo sauti.



    "Aaaaaaaaaaaaaaaaaeeeeeeeeehh!!" kelele hizo ziliambatana na Tereza wa ajabu kufumbua macho ghafla kisha kukikodolea kile kiumbe. Muda huohuo kule kwenye himaya ya Dr lee, Tereza akajitikisa kisha kimya akatulia. Sura yake ilionekana kubeba huzuni kubwa sana japo ililazimisha tabasamu.



    "Huna......huna.....huna budi.....budi.....budi....budiiii!" sauti nzito ikasikika na isijulikane inapotokea, ilikuwa ni ya kiume. Viumbe hao wawili walikuwa bado wanatazamana, moja alikuwa katika mshangao na huyu mwengine asijulikane yupo katika hali gani kwani hakuwa akionekana sura yake vizuri. Kimya kingine kikaibuka kisha kile kiumbe kisichoeleweka kikalikamata tumbo lake kwa mkono mmoja kisha akajikunja mithili ya mtu anayetaka kuchuchumaa. Alipokuja kukunjuka, ilikuwa ni kwa kasi sana kisha akarusha kitu kama kivuli kilichotoka tumboni mwake ambacho kiliingia tumboni mwa Tereza wa ajabu na kupotelea humo. Kwa kasi ileile ya ajabu, kile kiumbe kili msogelea Tereza wa ajabu kisha akalikamata tumbo la binti huyo kwa nguvu nyingi sana hadi alipokuja kuliachia, Tereza yule wa ajabu alikuwa akitoka damu kwenye pembe za macho yake, alikuwa akilia Tereza huyo wa ajabu lakini alilia machozi ya damu. Kile kiumbe kisichoeleweka, kikalegea na kudondoka kisha kupotea na kumuacha Tereza palepale chumbani. Ilikuwa tayari ni alfajiri ya siku ya tano ya kuhakikisha Dr. Henry anapeleka majibu mazuri kwa bosi wake. Alikurupuka kutoka ofisini kwake, alilala ofisini siku hiyo bila kupenda kwa ajili ya kuchanganyikiwa. Hadi inafika muda huo wa alfajiri hakuwa na amani juu ya kutimia kwa ahadi yake kwani alishindwa kabisa kulijua tatizo ni nini linalosababisha binti yule hadi kufikia muda ule asirudiwe na fahamu. Ametibu watu wengi kama yeye na walipata nafuu kwa muda wa siku tatu ama nne na hiyo ndiyo sababu ya yeye kujiaminisha na kuomba kupewa siku tano tu za kuhakikisha anayarudisha maisha ya Tereza duniani. Sasa maji yalikuwa yamefikia shingoni hapo yalibakia kumfunika tu na kummeza kabisa kisha kumpoteza kwenye mgongo wa dunia. Hakukumbuka hata kunawa maji ya uso, alivyokurupuka tu, moja kwa moja hadi kwenye chumba alicholazwa Tereza. Ile anafungua mlango wa hicho chumba, nusura aufunge na kukimbia, laiti kama isingelikuwa ni ujasiri na roho mbaya aliyonayo haki ya manani angelikimbia hapo kama mwehu. Alimkuta Tereza amekaka kitako kitandani akiwa bado anamipira iliyokuwa ikimsaidia kupeleka chakula mwilini mwake, dripu za damu na maji zikiwa bado zinafanya kazi huku lile bandeji kubwa likiwa lipo kichwani mwake kama ada. Dr. Henry alisimama mlangoni kwa muda sana asiyaamini macho yake juu ya kile akionacho. Aliivua mawami yake na kuivaa si chini ya mara tano lakini bado hakuibadilisha hali aliyoikuta mahala hapo.



    "umeamka kweli?" aliuliza lakini hakupata jibu kutoka kwa binti yule ambaye alikuwa ni kama ndiyo anaiona dunia kwa mara ya kwanza katika maisha yake.



    "Boo! Hasemi....lakini ameamka kweli bwana...oo my God mbona siamini sasa, ameamkaje huyu?" alikuwa amechanganyikiwa Dr. Henry, hali ile aliyoikuta ilimtisha sana hivyo hakuthubutu kumsogelea huyo binti mahali hapo bali alinyanyua simu na kumpigia msaidizi wake ......



    e akamwambia afike hapo mara moja. Msaidizi huyo alipofika, naye alishangaa sana kuona kuwa binti yule ameamka, hapo walikuwa na furaha kubwa kwani walikuwa wanauhakika wa kuishi tena. Hofu iliyowavaa tena ilikuwa ni vipi kama atakuwa amechanganyikiwa kiakili. Hawakutaka hilo nalo litokee hapo hata kidogo kwani endapo lingetokea basi ingekuwa ni balaa zaidi kuliko hata hilo la kwanza. Walimsogelea wakamchomoa kila kitu kisha wakamtoa mahali hapo na kumungiza kwenye chumba kingine huko walimfanyia vipimo mbalimbali. Walitoka na furaha ya aina yake baada ya kugundua kuwa binti huyo amepona kabisa japo bado jeraha la mshono lilikuwa halijaacha kutoa damu lakini hakuwa na madhara makubwa kama yale waliyokuwa wakiyahofia.



    "Boss, mgonjwa ameamka" alisema Dr. Henry akiwa mbele ya Bencov na Dr. Lee. Hakupata jibu bali alitazamwa kwa macho makali sana ya mshangao usiokuwa na imani.



    "Hebu rudia ulichokisema Dokta" aliongea Bencov huku Dr. Lee akiwa kama Paka mbele ya mtu au watu wanaokula kwani alikuwa akigeuza macho yake kama ya Mamba kila sauti ilipokuwa ikitokea, hakuamini hata kidogo hicho kilichokuwa kikiongelewa hapo.



    "mgonjwa ameamka na yuko salama kabisa" akarudia Dokta.



    "hapana hawezi kuwa salama hata kidogo, hata huko kuamka siyo kweli huo ni uwongo wa kuogopa kifo tu kwa kuwa leo ni siku ya mwisho kwako kama binti huyo asipoamka. Ataamkaje leo sasa kama sio kutuongopea huko" aliongea Dr. Lee kisha wote wakamtazama Dr. Henry aliyekuwa amenyoosha mikono yake mahali ulipo mlango wa kuelekea kwenye chumba kingine maalumu ambacho alikuwa amehifadhiwa huyo mgonjwa wao. Bencov hakungoja kitu kingine aliondoka hapo kwa kasi kubwa huku Dr. Lee akiiruhusu Baiskeli yake kupitia njia nyingine wote wakakutana kwenye chumba hicho kilichokusudiwa. Macho yaliwatoka wasiamini walichokikuta mule ndani. Walimkuta Tereza akiwa mezani akipata kifungua kinywa kizito sana asubuhi hiyo. Maswali yakajaa mengi vichwani mwao. Ni kweli huyu alikuwa mgonjwa aliyelala bila kujitambua kwa muda wa siku tano? Hapana kama....mbona haoneshi kama alikuwa ni mgonjwa sasa? Hayo yalikuwa ni maswali ya Bencov kutoka kichwani mwake lakini kwa Dr. Lee na Lady Devil kulikuwa na zaidi ya hayo. Kila mmoja alikuwa na lake kichwani na waliyokuwa wakiwaza wao si mambo ya hapa duniani. Waliamini kabisa huyo Tereza alikuwa amechukuliwa na King Bondo na si kitu kingine.



    "umesema hana matatizo ya akili?" Bencov alishindwa kuyahimili maswali yaliyokuwa yakikiumiza kichwa chake kwa wakati huo hivyo akaamua kuuliza. Dr. Henry akajibu kwa tambo kubwa kuwa akili bado hajampima lakini Tereza hapo alipo hana tatizo lolote bali amepoteza kumbukumbu zote za nyuma na hapo ni kama anaishi upya. Majibu hayo yakafanya matabasamu ya furaha ya Bencov na watu wake kufifia na kupotea kabisa. Halikuwa ni jambo la kulifurahia tena, kama Tereza amepoteza kumbukumbu waliamini hata uwezo wake wa kitaaluma pengine utakuwa umepungua. Ni hatari sana kwao na wasingetimiza matakwa yao kwa wakati pangilifu. Wafanye nini ili kuhakikisha kazi yao inakwenda kukamilika na kuwa imara.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Mbona kama kila tunalolifanya linakumbwa na kauzibe?" aliuliza Bencov akiwageukia wenzake lakini hakukuwa na aliyejibu hata mmoja badala yake Merina alimgeukia Dr. Henry na kumuuliza.



    "Hii hali itakuwa hivi kwa muda gani?"



    "kiukweli huwa inachukua muda kidogo hadi kutengemaa" alijibu Dr. Henry.



    "Hakuna njia nyingine mbadala ya kuweza kuhakikisha anatekeleza kazi yetu kwa haraka?" aliuliza tena Merina lakini kabla hilo halijajibiwa, Bencov akaingilia kati na kusema kuwa haamini kama huyo binti amepoteza kumbukumbu kwani kwa maelezo ya Dr. Henry wakati anamfanyia oparesheni alisema kuwa hakuna madhara makubwa yaliyopatikana kwenye ubongo sasa iweje apoteze kumbukumbu, yeye alihisi huwenda kuna tatizo jingine huwenda labda ni kuongea pengine kwani tangu wameingia hapo hakuweza kujibu swali lao hata moja. Alipomaliza kusema hivyo ahisivyo yeye, akamalizia.



    "nadhani kwa sasa amemaliza kula hebu tumpeleke kwenye chumba ambacho baba yake yupo na kwa muda huu ndiyo yale maumivu yanamrudia ambayo huwa yanadumu kwa muda wa dakika tatu, huko ndiyo tutajua kama tatizo ni kumbukumbu au kuna jingine", wote hapo wakaliafiki hilo jambo. Wauguzi wakaambiwa wamchuke kisha wakampeleka kwenye chumba ambacho alikuwa amehifadhiwa Backa. Walipofika huko walimkuta Backa akiwa katika maumivu makali sana alikuwa amejikunja kama upinde huku akitoa ukelele wa hatari sana. Mishipa ilikuwa imemtoka mwilini ikiwa imechora ramani ya kutisha sana mwilini mwa huyo bwana. Kilio alichokuwa akikilia huyo bwana kilidhihirisha dhahiri kuwa hakuwa akipitia maumivu ya kitoto. Hakuwa akitulia kitandani hata kidogo, sumu ile ilikuwa ikimfanya aishi katika shida kubwa sana. Tereza alisimamishwa mbele ya baba yake huyo huku akiwa ameshikwa na wauguzi wawili huku na huku. Hali ile ya baba yake pale kitandani ilionesha kumkumbusha kitu fulani lakini hakuweza kufanya kitu chocho bali ni machozi tu ndiyo yaliyokuwa yakimtoka mfululizo hii ilionesha kuwa bado alikuwa na kumbukumbu lakini huwenda kuna tatizo la kuongea pamoja na kusikia.



    "kumbukumbu ziko sawa. Dr. Henry hakikisha unakwenda kumfanyia vipimo ili tujue kama anasikia pamoja na kuongea kisha majibu tutayahitaji punde" alitoa maagizo Bencov kisha wakaondoka hapo chumbani. Tereza alitolewa kwa nguvu baada ya kuonesha hali ya kugoma. Akapelekwa chumba chenye mashine maalumu ya Checkup ili kuweza kujua tatizo lililopo kwa binti huyo. Baada ya saa moja Dr. Henry alipeleka majibu kwa mabosi wake kuwa binti huyo anamatatizo ya kuongea na kusikia na hataongea hadi mwisho wa maisha yake ikiwa ni pamoja na kusikia pia. Pumzi za furaha zikawakumba watu hao kuona kuwa kumbe hakuwa amepoteza kumbukumbu bali ni kusikia na kuongea tu, hilo lilikuwa siyo tatizo kwao.



    "tutatumia maandishi ama vitendo kumuelekeza nini tunataka" alisema Dr. Lee kisha akaagiza kuwa wamuache apumzike kwa siku mbili kisha wanaingia kazini rasmi.



    **********

    **********



    Ulikuwa tayari ni usiku umeanza kuingia na kichwani mwake kulikuwa na mambo matatu ya msingi lakini kuna moja hili liliongezwa na mtu aliyekuwa akimhoji muda si mrefu nalo ni kuhusu binti aliyemuuwa kijana mmoja kule kwenye vyoo vya baa. Aliamini kama atampata huyo huwenda kazi yake ikawa rahisi zaidi lakini kitu kigumu na asichokijua ni jinsi ambavyo angeweza kukutana na binti huyo. Roi alikuwa katika mkanganyo mkubwa sana wa mawazo hakujua lipi ni lipi na lipi lafaa kuwa la kuanzia. Alitoka mule chumbani kwake na kuelekea kwenye mgahawa wa pembeni ya hoteli hiyo aliyofikia ikiwa ni kwenda kujipatia chakula kizito sana usiku huo kutokana na tumbo lake kukosa chakula kwa muda mrefu. Alichagua sehemu tulivu kisha akavuta kiti na kujikalisha, akapokea menyu ya chakula akaisoma baada ya sekunde kadhaa, akaibuka muhudumu mmoja mrembo sana huyu alikuwa msichana nadhifu sana mwenye umbo nene kidogo.



    "Habari yako?" alisalimia huyo muhudumu kisha akauliza shida ya mteja huyo baada ya kuijibu salamu yake kwa utulivu mkubwa. Roi aligusa namba ya chakula alichohitaji kisha muhudumu huyo akaondoka. Alitulia hapo kwa muda kidogo akisubiri chakula alichoagiza, alikuwa ametulia sana na hakuhitaji kitu chochote kile alitaka kusubiri tu huku macho yake yakitazama luninga kubwa kabisa iliyopo ukutani. Hakuwa akitazama luninga pekee bali hata warembo wanaoingia na kutoka alikuwa akiwaona, alipenda sana totozi Roi hivyo hakuacha kuyaburudisha macho yake kwa kuwatazama. Alipokuwa ametulia hapo, mlangoni kukaingia binti mrefu, mweusi kiasi mwenye umbo tamu sana lililojiachia vema sana kuanzia maeneo ya kiunoni kuja chini, alikuwa na umbo namba nane huyo dada aliyeingia hapo. Roi alimtazama kwa muda sana na kwa vile alikuwa amejituliza sehemu ambayo si rahisi kumuona, aliweza kumsanifu vizuri sana binti yule. Picha ya binti aliyeelezewa na Tamimu ikajichora kichwani kwake. Ndiye mwenyewe huyu. Aliwaza. Chakula kikaletwa akajisafisha mikono vizuri na kuanza kula. Ulikuwa ni ugali wa muhogo na Samaki wa maji baridi wa mchemsho waliokolea Limao. Macho yake hayakuacha kumtazama yule binti lakini alipoangalia kwa muda huo alishtuka, ni baada ya kukutanisha macho yao na binti yule. Dada huyo alionekana kupigwa na butwaa sana kama kuna kitu kilikuwa kinamshangaza kwa kijana yule. Hawakudumu sana katika kutazamana kila mmoja akaendelea na shughuli zake japo kila mmoja alikuwa akigeuka kwa nafasi yake.



    "Dada samahani kidogo" aliita Roi. Dada aliyeitwa akasogea kwenye meza ya kijana huyo akiwa tayari kusikia kile alichoitiwa.



    "Samahani unaweza kunambia yule binti kiasi anachodaiwa?" ahaa! Yule pale aliyevaa kitop cha pinki?"



    "ndiyo"



    "ni shillingi Elfu kumi na tano (15,000)." alijibiwa Roi kisha akasema kuwa bili yote atalipa yeye. Yule dada akaondoka. Roi alikula alipomaliza alilipa kila kitu kisha akatulia hapo akipoteza muda, yule dada alipotaka kulipa aliambiwa kuwa bili imeshalipwa tayari, alipouliza na nani, akaoneshwa kiti ambacho huyo kijana yupo. Akashangaa lakini hakusema kitu akajikuta akitabasamu tu kama kawaida yake. Huyo alikuwa ni Petii. Hakupoteza muda mahali hapo alipohakikisha kuwa hadaiwi, alitoka nje ya huo mgahawa lakini muda huo huo Roi nae akatoka nje kwa kuvizia hakutaka kuonekana kirahisi na binti yule kama anamfuatilia. Petii aliingia kwenye gari moja nyekundu kisha kuondoka eneo lile. Roi hakutaka kumuacha aliingia kwenye gari aliyo ikodisha safari ya kumfuatilia ikaanza. Ulikuwa ni mwendo mrefu sana lakini hakuchoka kumfuatilia binti yule na safari hiyo iliishia kwenye Jingo moja kubwa sana lililokuwa liking'aa kwa mataa mengi ya kuvutia, lilikuwa likisomeka kwa juu MUAVENGERO CASONO. Alishuka binti huyo kisha kupiga hatua za taratibu sana kuingia ndani ya kasino hilo. Muziki ulikuwa ukipiga kwa taratibu sana aliingia hadi ndani kabisa mwa kasino hilo. Michezo mbalimbali iliyokuwa ikichezwa na matajiri wakubwa kama Pokker na mingi mingine ilikuwa ikiendelea kama ada. Kulikuwa na makundi makubwa ya matajiri mule ndani kila kundi lilikuwa na burudani yake hiyo ndiyo ilikuwa kawaida ya kasino hilo kila siku ya mungu.



    "Huwezi kunizidi kirahisi kijana sisi ni wakongwe kwenye huu mchezo na hatujauanza leo" alibwata mzee mmoja aliyeonekana kuwa ni Tajiri sana.



    "ha ha hahaaa! Bwana mkubwa unajidanganya, tunafanya hili gemu kwa muda gani?" aliuliza huyo kijana, muda wote huo Petii alikuwa ametulia kimya kwenye kiti kimoja kirefu akiwa anajipatia kinywaji kikali sana huku akiufuatilia ule mchezo wa Pokker uliokuwa umeanza kwa mabishano na matajiri wawili.



    "dakika si kitu, kinachotakiwa mshindi aonekane" alijibu yule tajiri mzee.



    "nini unaniahidi au unaweka mali gani nikishinda hili gemu?" aliuliza tena yule kijana.



    "ukishinda hili gemu kijana, ninakupa binti yangu huyo hapo lakini ni lazima na wewe uniahidi kuwa nikishinda mimi unanipa nini?" alijibu kisha akaacha swali mezani. Yule kijana kabla ya kutoa jibu alimtazama kwanza binti aliyetakiwa kumchukua kisha akageuza shingo lake kutazama kwenye Parking kubwa ya magari ambayo ilikuwa ni V.I.P. Kulikuwa na gari moja ya kifahari sana aina ya Doll. Macho ya watu wote pale yakaelekea kwenye hiyo gari. Ilikuwa ni gari ya kifahari sana ambayo ni huyo kijana pekee aliyekuwa akilitumia kwani gari hiyo ilikuwa ikitumiwa zaidi na Masuper star pekee wa huko ughaibuni kama Thihenry Henry, ilikuwa ni ajabu sana kijana huyo kutoa kitu cha thamani kama hiyo gari na ilikuwa ni dharau kubwa kwa bosi huyo, aliona kama anadharauliwa na huyo kijana mahali hapo.



    "kwani huna kitu kingine cha kutoa hadi ile gari kijana?" aliuliza huyo tajiri mzee.



    "Pia naona thamani ya hiyo gari ni ndogo sana ukilinganisha na urembo alionao binti yako.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Binti yako ni mrembo sana na nitajivunia kuwa nae" alijibu tajiri huyo kijana. yule tajiri mzee akamtazama binti yake ambaye muda wote alikuwa katika tabadamu pana kisha akageukia mchezoni. Mchezeshaji akaanza kuchezesha. Mambo yalikuwa magumu sana hapo na kila mmoja alitegemea ushindi lakini mzee yule aliona dalili zote za kushindwa kwani yule kijana alikuwa ni hodari sana wa kucheza huo mchezo. Roi alikuwa ametulia kimya kwenye kona fulani isiyoruhusu kuonekana na kiumbe yoyote yule, alikuwa na chupa kubwa ya mvinyo akiwa anajibanjia taratibu kwenye gilasi. Alijua kuwa kwa muda wowote ule mahala hapo patakuwa si salama hata kidogo na kila akimtupia macho Petii alikuwa akijua fika kuwa binti yule hakufika bure mahala pale, ni lazima kutakuwa na kitu alikifuata. Kelele za wastani ziliibuka huku yule tajiri kijana akiwa na furaha kubwa mahali hapo, yeye na vijana wake watatu pamoja na walinzi wake wawili walikuwa tayari kuondoka akiwa amemshika yule binti mkono.



    "unajiamini sana kijana na unaonekana ni mahili sana huogopi kitu wewe?" aliuliza yule tajiri mzee.



    "sijawahi kuogopa na hakuna kitu cha kuniogopesha" alijibu yule tajiri kijana. Tajiri mzee yule aliuma meno kwa hasira kali sana hakuwa mtu wa kushindwa kipumbavu vile sasa ni kwanini kashindwa tena akiwa amemuuza binti yake kipenzi kwa gharama nafuu kiasi kile. Akiwa anajiuliza hili na lile, mara kukaingia mtu mule ndani. Huyu alikuwa ameongozana na mtu mmoja aliyekuwa amejazia misuli. Aliingia pale ndani kisha akajikalisha kwenye kiti kimoja karibu kabisa na tajiri yule mzee. Hakukuwa na salamu yoyote mahali hapo bali alimtazama yule mzee kisha akamuuliza.



    "Aisee rafiki, umekuja mwenyewe leo?" yule tajiri mzee akasema hapana nimekuja na binti yangu lakini....!" hakumalizia yule mtu aliyeingia hapo ndani akamkatisha.



    "nilikuwa nataka kushangaa, Bande Sir hakuwahi kumuona rafiki yake kipenzi akiacha kutembea na jicho lake, njoo hapa binti yangu mbona umesi......!"



    "huyu hayupo kwenye amri yenu tena huyu ni mali yangu kwa sasa na ninaamri naye" alijibu kwa jeuri kubwa yule kijana, hali ile ilimshangaza sana bwana huyo, waziri wa ulinzi na usalama Mh. Bande Sir. Akajikuta akiuliza kwa mshangao mkubwa.



    "huyu ni nani anayethubutu kunikatisha maongezi yangu.....wewe, hata kama sina mtoto hata mmoja lakini kama ningetaka kuzaa ningekuwa na Panya mkubwa tu wa kijivu kama wewe mwendawazimu" alisema kwa hasira kuu sana kisha akasimama na kutaka kumchapa kofi lakini alikumbana na kizuizi kizito sana kutoka kwa walinzi wa kijana yule. Macho manne makini yakawa yanatazama kwa namna yake mahali hapo. Mawili yakiwa yanamtamani Bande Sir na mawili yalikuwa yakihitaji kujua kitakachotokea mahali hapo ili kuweza kupata pa kuanzia. kitendo kile cha kupokea kizuizi kilikuwa ni kibaya sana kwake, aliziona dharau za yule kijana waziwazi.



    "Kunguru wawili kwenye kapu!" alipiga kelele kisha muda huo huo wale walinzi walioleta pingamizi la kupigwa kofi bosi wao, wakapokea risasi za kichwani muda huo huo wakadondoka chini.



    "Hivi unadhani mimi ni mjinga si ndiyo, unadhani nilikuwa sioni kinachoendelea hapa? Nilikuwa naona na nilijua ni lazima uibuke mshindi lakini sasa sisi hatujawahi kupoteza. Kila mshindani atakayeingia humu ni lazima ashindwe hakuna anayeweza kushinda humu mjinga wewe" Bande Sir aliwaka sana alikuwa kwenye hasira kali mno. Wakati akiwa anazidi kutamba hapo aliuchomoa mkono wake mmoja na kutaka kumpiga yule kijana kwa mara nyingine tena lakini mkono ule ulizuiliwa kwa umaridadi mkubwa sana. Wale vijana watatu wa yule Tajiri kijana, walizuia tena. Hili likawa kosa kubwa zaidi. Kwenye kona moja ya eneo lile, wakaamka vijana watatu. Wakapiga hatua za taratibu hadi walipo wale vijana na huyo bosi wao. Mkono ukatembea huku Bande Sir akiwa amerudi pale kitini akitingisha mguu. Wale vijana walichezea kichapo kwa muda mfupi tu wote wakawa chini wakiwa maiti, akabaki yule tajiri peke yake akiwa na hofu kubwa sana. Petii aliutazama ule mchezo akaona ulinzi wa pale haukuwa mdogo akajua hawezi kufanya kitu kwa huyo Bande Sir lakini akikumbuka kuwa amepoteza muda mrefu sana bila kumkaribia adui huku mkuu wake wa kazi akimuona mzembe, aliona kuwa hapo iwe isiwe ni lazima amuweke huyo bwana chini ya ulinzi. Wakati Bande Sir akiwa ananyanyuka pale kumsogelea yule kijana Tajiri, Petii alikuwa ameshausoma mchezo na kujua ni walinzi kiasi gani ambao walikuwa wapo hapo pia alijua ni wapi na walikokuwa wamekaa. Kitendo bila kuchelewa alijirusha akiwa na bastola mbili mkononi mwake huku zikiwa zinawadondosha walinzi kadhaa waliokuwa wamejificha sehemu ambazo si rahisi mtu kujua. Hofu kubwa ikaibuka mule ndani yule tajiri mtoto akaona huo ndiyo mwanya wa yeye kuweza kukimbia kweli alifanikiwa, akakimbia yeye na mali zake Lakini huku ndani ilikuwa ni balaa kubwa lililokuwa limeanzishwa na Petii. Alidondosha wengi kisha alipoona hapo wamebakia wachache, aliruka nyuma ya Bande Sir akamuwekea chuma cha kichwani.



    "Ukochini ya ulinzi mwanaharamu wewe" aliwaka Petii akiwa makini sana kuwatazama watu waliopo eneo hilo. Ukumbi wote uliharibika, badala ya burudani sasa uligeuka ukumbi wa damu na mauwaji. Roi alikuwa akifuatilia matukio yote yaliyokuwa yakiendelea hapo bila kujulikana kwani tayari alikuwa ameshajichanganya na kundi kubwa la watu.



    "Umekuja hadi huku wewe mwanamke, nadhani sasa umekuja kunipa roho yako au?" aliongea kwa dharau kubwa sana Bande Sir. Alikuwa akijua fika kuwa hakuna kitu kinachoweza kumuangusha mtu mkubwa kama yeye tena wa serikali.



    "nimekuja kuichukua roho yako kisha nipeleke taarifa nchini kwangu kuwa umeshakufa tayari" alisema Petii akiwa bado yupo makini sana lakini muda huo huo tukio moja la ajabu sana likajitokeza, lilikuwa ni la ajabu kweli. Askari polisi wengi sana walivamia mule ndani kisha wote wakamnyooshea Petii silaha zao huku wakimtaka amuache muheshimiwa na yeye akizisalimisha silaha zake. Hili neno Muheshimiwa ndilo lilimchanganya.



    "Muheshimiwa? Mtu aliyekuwa katili na mafia wa kulipwa aliyetoroka mahabusu kwa kuwauwa polisi akiwa kizuizini mara baada ya kusababisha mauwaji ya mtoto wa waziri mkuu Malawi, leo hii ni muheshimiwa?" alijiuliza Petii bila kupata jibu. Alijua hapo kwa serikali hawezi kufanya kitu, akabidi kuwa mpole tu, aliiweka silaha yake chini kisha akajisalimisha. Bande Sir aligeuka na kumtazama binti huyo kisha akamwambia.



    "Uliweza kunitia mikononi ukiwa nchini kwenu lakini huku umekifuata kifo, utakufa bila kelele kima wa kike wewe" alipokwisha kusema hayo akamtazama kwa macho mabaya sana kisha akamalizia.



    "mimi ndiyo Bande Sir kama hujui. Mimi ndiye niliyesababisha kifo cha yule malaya mtoto wa waziri wa nchi yako baada ya kulipwa pesa nyingi na muasi mmoja wa serikali yenu. Sikuwa na kosa, mimi nimelipwa, nikatumwa kazi kisha nikafanikisha. Wewe na serikali yako mkatuona sisi watatu ni wauwaji kwa kuwa tumeuwa mtoto wa waziri. Mkatutia mbaroni nasi kwa uzembe wenu tukatoroka. Nashangaa umekuja huku. Ile kesi iliisha kule na huku ni maisha mapya......hey mpelekeni huyu binti kwenye chumba chenye hewa safi akapumzike" alipomaliza kujitapa mbele ya yule binti, akaagiza vijana wake ambao walikuwa ni tofauti na wale askari kuwa wampeleke binti huyo chumba chenye hewa safi. Petii alikuwa na mawazo sana juu ya mtu huyo alishindwa kujua ni mtu gani kwenye taifa hilo. Kwanini basi polisi hawakumchukua yeye na achukuliwe na vijana wengine wasio polisi? Alikuwa akijiuliza sana Petii. Haikuwa kwa petii peke yake bali hata Roi hilo swali alikuwa akijiuliza kuhusiana na uwongozi wa nchi hiyo ni kwanini hayo yalikuwa yakitokea kirahisi hivyo.



    "Yule ni nani mwenye mamlaka ya kuwaamrisha askari wamtii kiasi kile?" alijiuliza sana Roi lakini jibu hakulipata. Alitoka kule ndani akaelekea kwenye gari aliyokuja nayo Petii akaipekua lengo ikiwa ni kujua yule binti ni nani, akapekuwa hapa na pale baada ya kufungua mlango wa gari ile kwa njia zake binafsi. Hakuna kitu cha maana sana alichokipata. Alizidi kupekuwa hadi aliporidhika tayari alikuwa amepata kitu kilichokuwa kimempa maelekezo fulani. Akatoka na kuiacha ile gari hapo hapo akaingia kwenye gari yake na kurudi hotelini kwake.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kichwa kilikuwa kikimuuma sana Roi, haya matukio yalikuwa yamepandiana kiasi kwamba aliona huo mzigo ni mkubwa tena ukielekea kumuelemea pengine. Alikuwa amesimama katikati ya chumba cha binti Petii hiyo ikiwa ni baada ya kupata muongozo kutoka kwenye upekuzi wake kwenye ile gari. Alikuwa anajina kamili la yule binti pili akiwa na kila kitu pamoja na mengine mengi ya msingi yanayomhusu binti yule.



    "Kumbe ni mpelelezi kutoka Malawi? Amekuja kupeleleza nini hapa Ungamo? Na ni kwanini alimuweka yule bwana chini ya ulinzi kule Kasino? Ni nani yule bwana?" alijiuliza maswali mengi lakini aliona pengine maswali yake yanaweza kupungua iwapo akifanya kitu fulani. Macho yake yakaangukia kwenye kompyuta ya mapajani iliyoko ndani ya kabati. Akaitoa na kuanza kuiwasha kisha kuingiza nywila za kughushi kwa vile ajuavyo mwenyewe, kwa utaalamu wake alionao alifanikiwa baadhi ya mambo lakini kuna mambo yalimuwia ugumu kidogo. Kuna file moja hilo lilikuwa limefungwa madhubuti sana kiasi cha kushindwa kulifungua. Akajua bila shaka hilo litakuwa linamambo ya msingi zaidi. Akanyanyua simu yake kisha akatuma ujumbe mfupi wa maneno kwenda kwa mtu fulani. Ujumbe huo ulikuwa umebeba code maalumu za kompyuta ile ambazo zingeweza kumsaidia mtumiwaji kuitambua kompyuta hiyo ili ajue nini cha kufanya.



    MOROGORO NCHINI TANZANIA.



    Ndani ya ofisi ndogo sana ambayo haikujulikana ipo maeneo gani. Ilikuwa ni ya siri sana kiasi kwamba hata raisi wa nchi hakujua ofisi hiyo ilipo. Japo alijua uwepo wa vijana hao lakini mahali wanapofanyia kazi ilikuwa ni ngumu sana kujua hii ilifanyika hivi kwa sababu za msingi sana, hawakutaka kuharibu utendaji wao wa kazi kwani walijua fika kuna Ofisi nyingi za kipelelezi hivyo waliogopa kuharibiwa hata na wapelelezi wenzao ukizingatia ofisi ndogo kama hiyo imeweza kupewa kazi kubwa kama hiyo. Si kutambulika ilipo tu bali hata jina la ofisi hiyo lilikuwa bado ni kitendawili. Amiri alikuwa ametulia kwenye kiti chake cha kiofisi akifanya haya na yale mara kwenye simu yake kubwa ya kisasa na aipendayo, kukaingia ujumbe mfupi wa maneno ambao ulikuwa umebea kodi maalumu na ujumbe huo ulikuwa umetumwa kitaalamu kwa namba maalumu pia. Amiri aliufungua haraka haraka kisha akaanza kuupitia, alijua nini alitakiwa kufanya.



    "Father, nilisema kuwa kimya kingi kina mshindo" alisema Amiri alipokuwa ameiweka simu ya kiofisi sikioni kisha akasema tena baada ya kusikiliza upande wa pili.



    "Roi yupo kazini sasa na kuna vitu amenitumia nimsaidie" alisema hivyo kisha baada ya muda akashusha simu na kuanza kazi ya kuziingiza zile Code kwenye compyuta yake kubwa. Akaanza kufanya yake muda mfupi tu alikuwa amemaliza kila kitu na kulifungua hilo file lililokuwa likitakiwa kufunguliwa, alilipitia file lile kisha akatuma Code za kuweza kulifungua lile file kwa Mtaalamu wa mambo Roi.



    Chumba kilikuwa kinazizima sana, baridi ilikuwa kali kiasi kwamba Petii alikuwa ameanza kuhisi hali ya kufakufa ikimjia. Walikuwa ni makatili sana watu wale, walikuwa wamemvua nguo Petii na kumuacha na nguo ya ndani pamoja na sidiria pekee, alikuwa akiteseka mno lakini hakuwa na njia ya kuweza kujinasua kila akifikiria jinsi ambavyo angeweza kutoka mule ndani hakupata jibu. Mbaya zaidi hakuweza hata kutoa taarifa yoyote ile kwa watu waliomtuma kazi ile. Baridi ilizidi kumtafuna kwa kasi kubwa sana, alikuwa anahisi kuganda sasa. Mara ya kwanza alipoingizwa kwenye chumba hicho aliona ni hali ya kawaida lakini kila muda ulivyokuwa ukisonga ndivyo hali ilizidi kuwa mbaya. Alikuwa amefungwa vibaya sana, alikuwa amefungwa ile kamba kwa kutanuliwa miguu na mikono, ulikuwa ni unyanyasaji mkubwa sana uliokuwa ukifanyika mahali hapo. Kila muda baridi ilizidi kuongezeka hadi akapoteza fahamu kabisa na kushindwa kujua nini kilichokuwa kikiendelea. Alipokuja kuzinduka hali ilikuwa ni ya joto la wastani ile baridi haikuwepo tena, japo alihisi maumivu ya hapa na pale yaliyokuwa yakimsumbua. Alijiona yuko na ahuweni lakini bado alihisi mateso kwake yataendelea kuwa makubwa sana kutokana na roho ya watu waliomteka zilivyokuwa mbaya.



    Alitulia mule ndani na hakukumbuka kama alishawahi kupewa chakula tangu kuingia mule ndani. Njaa ilikuwa ikimsumbua sana na hata tumbo lilikuwa likimpa lawama kuwa halikupata kitu kwa masaa kadhaa. Angefanya nini sasa wakati yupo kwenye mikono ya mtu katili, mtu ambaye hakuwahi kuuona wema wake tangu kumfahamu. Alikuwa yuko pale kwa rehema za Mungu tu lakini si kwa uweza wake mwenyewe. Alishajikatia tamaa tayari ya kuweza kujinasua mahali hapo, kila akiziangalia kamba alizofungiwa ndiyo alizidi kuchanganyikiwa kabisa. Mlango wa kile chumba ulifunguliwa wakaingia watu wawili. wote hao aliwafahamu kwa sura kwani walikuwapo siku akiwa anawekwa chini ya ulinzi na jeshi la polisi lisilo na sauti kwa watu hao.



    "tazama pembe ile, umeona nini? Tazama na kule, tena tazama kwa umakini mkubwa, umeona? Ile ni mifupa ya binadamu wajinga kama wewe msiojua hatari na heri. Wajinga wenzako walikufa kama ambavyo utakufa wewe. Sikupigi ngumi wala kukuchoma mkuki. Kinachofuata ni wewe kupambana na baridi kali sana hadi unakufa malaya wewe. Hivi kwanini mnafuatilia vitu vilivyo nje ya uwezo wenu? Kwanini hamujihurumii, tazama wamekutuma wewe mwanamke mrembo kabisa, mwanamke mzuri mwenye kila sifa ya kukata vitunguu kwa ajili ya kumuandalia bwana wako chakula cha usiku kisha utandike kitanda kwa ajili ya kumburudisha mumeo" alisema kwa kujitapa sana Bande Sir, mtu katili sana ambaye kitu kuuwa kwake ni kama kumpa kuku uwele kisha kumkamata na kumchinja. Maneno yale yalikuwa ni kero kubwa sana kwa Petii lakini hakuwa na jinsi ya kufanya. Uwanaharamu wa bwana yule ni mkubwa sana hivyo kupata kujinasua hapo ni ndoto kubwa kwake. Bwana yule alikuwa akitamba chumba kizima kwenda huku na kule ndani mule. Hali hiyo ilizidi kumpa hofu kubwa sana Petii.



    "Ni muda mrefu sana hiki chumba hakijamdondosha mtu kisha kuikausha damu yake, nafarijika kuona kuwa leo kinafanikisha kitu ambacho pengine kilikuwa na hamu nacho sana kukifanya, nikutakie kifo kizuri cha kuganda kwa damu yako mwilini, huu ndiyo muda wa baridi kali sana ambayo itakuondoa duniani" aliongea Bande Sir kisha akatoka mule ndani. Kitendo cha yeye kutoka tu ikawa ni kama ameiruhusu baridi ianze kuleta mateso mwilini mwa binti yule.



    **********



    Gari ndogo Toyota Carina ilipiga breki mbele ya ofisi kubwa ya makao makuu ya polisi mida ya saa saba na nusu adhuhuri, Roi alishuka kutoka garini moja kwa moja alielekea kwenye mlango mkubwa wa kuingilia ndani ya ofisi ile. Alikutana na walinzi ambao walimzuia yeye kuendelea mbele kwani uendaji wake ilionesha kuwa moja kwa moja alikuwa akielekea kwenye ofisi ya IGP. Aliwatazama wale walinzi kwa nafasi kila mmoja kisha akawauliza kuwa nini sababu ya kumzuia wakati hata katibu muktasi wa bosi wao hajamfikia. Wale vijana wakajibu kwa jeuri kuwa hawana muda wa kuweza kujibishana nae kwani hapo walipo wapo kwenye majukumu yao ya kila siku hivyo anapaswa kusema shida yake na siyo kuuliza. Roi aliwaangalia tena kisha akawaambia kuwa alikuwa na shida na katibu muktasi wa IGP. Wale vijana wakamuuliza kwa shida ipi labda, hapo Roi akajua sasa hao vijana walikuwa wakielekea nje ya utaratibu hivyo akataka kupandisha hasira zake za wazi kabisa lakini punde alimuona mtu aliyekuwa akimuhitaji mahali hapo akitoka ofisini kwake, alikuwa akimpita hapo akionekana kuwa na haraka sana.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Mkuu nipo hapa kwa ajili yako nilikuwa nakuhitaji ofisini kwako" alisema Roi huku akiwa anawatazama wale vijana waliokuwa wapo kwenye hofu kidogo, alikuwa akiwatazama kwa macho yaliyodhihirisha kukerwa na ile tabia ya kumuwekea kizingiti cha kushindwa kuonana na mkuu wao wa kazi. IGP alimtupia macho huyo kijana kwa muda kidogo, akagundua kitu fulani kutoka kwa kijana huyo, alichokifanya ni kumruhusu kijana huyo kuingia kwenye ofisi yake ili kuweza kujua shida yake. Walirudi ndani kisha wakatazamana kwa muda kabla ya kuanza kuongea chochote mahali hapo. Kimya hicho kikapelekea IGP kuanza kuuliza shida hasa ya kijana huyo kufika hapo ofisini kwake. Roi alimtazama bwana huyo aliyechafukwa na vyeo vingi vya kipolisi kisha akashusha pumzi nyingi sana kabla ya kukifungua kinywa chake.



    "Inspekta, inavyoonekana kwenye nchi hii kuna watu wanasauti kubwa kuliko jeshi au wanausalama wa nchi hii?" aliuliza Roi, IGP swali hili lilimshtua sana, lilikuwa ni swali la mtego sana hakukurupuka kulijibu kamwe, alitulia kimya kidogo ili kuweza kulitafakari hilo swali kwa kina lakini kwa haraka sana. Ni kwanini ameulizwa hivyo na mtu huyo aliyemuuliza swali hilo ambalo lilikuwa ni swali lenye maana mbaya sana kwa uongozi wake. Lilikuwa ni tusi kwa jeshi la polisi hilo swali, jeshi lilionekana zembe sana katika kutekeleza mambo yake na mamlaka yake kama jeshi kiasi cha kuwafanya watu waliojivika upapa wawe juu.



    "kwanini umeniuliza swali hili? Wewe ni nani kwani mwenye uwezo wa kuniuliza hivyo?" aliuliza IGP. Roi alitabasamu kidogo kisha akazungumza.



    "Inabidi na mimi niende kama wewe ulivyoenda Afande, samahani sana lakini. Nini kilifanyika kutoka kwa jeshi la polisi la nchi hii baada ya wale wapelelezi wawili kuuwawa? Sawa labda wale ni kwa sababu tu siyo raia wa Ungamo je, vipi kuhusu mfanyabiashara mkubwa ambaye alikuwa na sifa kubwa huku akiwa na nafasi ya pekee katika kuliingizia kipato kikubwa taifa hili?" ilikuwa ni kwa sauti ya chini sana kiasi kwamba hata kama kungekuwa na mfuatiliaji, asingeng'amua jambo. akaweka alama ya kuuliza hapo Roi kisha akatulia akiwa anamtazama IGP usoni. Mshtuko mkubwa ulimpata IGP, hili swali la safari hii lilikuwa likotofauti kidogo, hakuna mtu ambaye anaweza kuuliza swali hilo kiwepesi tu pasipo kuwa na sababu maalumu au kuwa mtu maalumu. Huyu ni nani? Akalifanya swali hilo kuwa linalojirudia kichwani mwake.



    "Ok, mkuu niko hapa kwa ajili ya kuhitaji msaada wako maana hali ilivyo sasa si shwari na ninahitaji kuwatia mikononi haraka sana waliowauwa ndugu zangu. Nahitaji ndege ndogo ya serikali iweze kusafirisha maiti za wale wapelelezi kuelekea Tanzania lakini pia kuna kitu cha pakee sana ninakihitaji kutoka kwako eidha vijana wako waweze kunisaidia", akaweka koma kidogo, akavuta pumzi ndani kisha akaendelea.



    "naitwa Rajabu Isihaq Omair. Ni mpelelezi wa siri kutokea Tanzania. Nimekuja kwako kutokana na upelelezi wangu wa awali na kujua kuwa wewe ni pekee utakayeweza kunisaidia. Nahitaji kujua muuwaji aliyesababisha kifo cha Ndungai" akatulia Roi akamtazama IGP aliyekuwa akikikodolea macho kitambulisho cha kijana huyo, hakuamini macho yake kama kijana huyo kwa muda mfupi tu aliofika hapo ameweza kugundua vitu vyote hivyo. IGP akaahidi kumsaidi kijana huyo hayo aliyoyataka ikiwa ni pamoja na kutoa hiyo ndege ya serikali ambayo itasafirisha hiyo miili ya wapelelezi wa Tanzania lakini pia alifungua mtoto wa meza yake akatoa karatasi mbili, moja ilikuwa ni ya uchunguzi wa wale wapelelezi, moja ikiwa ni ya mauwaji ya Ndungai, mfanya biashara mkubwa wa Taifa hilo la Ungamo lakini pia hakusita kumueleza kuhusu mauwaji ya ajabu ya askari waliokuwa lindo ambao waliuwawa kwa silaha za ajabu zisizoeleweka kisha kufa kifo kibaya baada ya kubaki kitandani kwa muda wa masaa Sabini na mbili (72). Kifo ambacho kila mtu kilimuacha akiwa mdomo wazi kwani walikuwa wakimung'unyuka na kubakia mafuvu tu na mifupa, haikujulikana sumu hiyo ni sumu au kemikali ya aina gani ambayo ilitumika kuwangaamiza askari wale. Roi vyote hivyo alikuwa akivifahamu baada ya kusoma magazeti kadha wa kadha lakini alikuwa mpole hapo pia ili kuweza kujiaminishia juu ya habari ile ya kuogopesha. Alipewa mambo mengi sana Roi hadi ambayo yalikuwa si dhahiri. Alichokifanya kijana huyo ni kumuomba IGP ashughulikie mambo ya kuisafirisha miili ile ikiwa ni sambamba na kuisindikiza uwanja wa ndege kwani yeye kuna kazi ya muhimu alikuwa akihitaji kuifanya. IGP hakulipinga hilo swala wakaagana huku wakilitaka jambo hilo kuwa siri kuliko usiri wenyewe, Roi alimtaka Inspekta Jenerali awe mkimya na asiseme chochote kuhusu ujio wake kwani sasa anaingia kazini rasmi, akatoka mule ofisini akiwa amebeba bahasha ya khaki. Roi alishafanya mawasiliano ya kutosha nchini Tanzania, alikuwa ameshatoa taarifa kuhusiana na ujio wa miili ya wapelelezi waliouwawa nchini Ungamo. Siku hiyo majira ya saa mbili usiku ndiyo muda pekee ambao watu wachache walio katika sare za jeshi la polisi walionekana hospitalini Pande kwa ajili ya kufanya shughuli ya kuichukua miili ya marehemu waliokusudiwa kuchukuliwa. Maeneo hayo alikuwa Roi kwa ajili ya kazi maalumu, alikuwapo hapo kwa ajili ya kuhakikisha kuwa hali ya usalama na usiri mkubwa inakuwepo lakini pia Inspekta Bogo alikuwepo eneo hilo ikiwa ni katika kuhakikisha suala hilo linafanikiwa bila kuwa na chokochoko zozote. Walijua fika kuwa kuna viumbe au kimbe kimewekwa hapo kwa ajili ya kuhakikisha kila kinachofanyika hapo kinatoka na kuwakuta mabwana wakubwa. Roi alikuwa amepiga mavazi meusi tupu kuanzia soksi hadi mkanda wa suruali, alikaa kwenye kona moja hivi ya kutokea chumba cha kuhifadhia maiti akiwa ameyakaza macho yake yasiache kutazama kila kisichoeleweka mahali hapo. Wakati shughuli hiyo ikiwa inaendelea, kuna binti mmoja yule binti mtoa taarifaa alikuwa maeneo hayo akiwa anashuhudia kila kitu mahali hapo ili kuweza kutoa taarifa ya yote atakayoyapata. Roi hakutaka kukaa mbali na binti huyo alimfuatilia hatua kwa hatua kuanzia pale walipoingia hadi kuingia chumba cha maiti. Alikuwa amejitenga sana huyo binti pia alionekana kuwa katika wasiwasi mkubwa kwani alikuwa hatulizi shingo yake. Yule binti baada ya kuridhika na udakuzi wake, alitoa simu yake ya mkononi kisha kusogea pembeni kidogo, akapiga namba fulani kutoka simuni mwake lakini wakati anaiweka sikioni tu, Roi akainyakua ile simu kisha kuitia mfukoni ikiwa tayari imekwisha kupokelewa. Yule dada akageuka kwa kasi kisha kurusha makonde mawili ambayo yalipishwa kama mchezo. Akatulizwa na ngumi moja kali sana iliyopigwa kwa kuzunguushwa mkono, ngumi hiyo ilitua kwenye kifua cha huyo binti. Maumivu aliyoyapata alikuwa ni lazima abweke lakini Roi alimzungukuka binti huyo akapiga ngumi nyingine ya kwenye mbavu, binti huyo akalegea. Roi alimvuta binti yule kwenye giza kidogo kisha kumuuliza maswali machache tu.



    "nani aliyekutuma kuja hapa?" lilikuwa ni swali la kwanza aliloulizwa huyo binti.



    "nimetumwa na serikali ya nchi hii?" alijibu kwa kiburi.



    "unamuda mfupi sana wa kuishi na kufa, ukiwa mkweli utaishi lakini ukiwa mkaidi utakufa" alisema Roi.



    "niuwe tu hata sasa kwani sina jingine la kujibu zaidi ya nililolijibu" alizidi kuongea kwa dharau kubwa sana binti yule lakini wakati yote hayo yakiwa yanafanyika ile sinu ilikuwa ikipeleka taarifa kwa mpigiwaji.



    "sahamahani sana mrembo, ungenikuta sipo kazini ningekusamehe kwasababu huwa sina desturi ya kuuwa warembo kama wewe lakini kwa kuwa nipo kazini I'm sory" aliongea hayo Roi kisha aliizungusha shingo ya huyo dada hadi ikatoa sauti ya mvunjiko akamuacha hapo chini bila kumsitiri akaondoka anapoajua yeye.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ilikuwa ni ripoti iliyokamilika kabisa na alipoisoma kwa umakini mkubwa alijua kuwa sura ya muuwaji haikuwa hiyo. Muuwaji alikuwa ni mtu makini sana kwani sura iliyokuwa ikisomeka pale kwenye picha ile ilikuwa ni ya mtu aliyetoka kumuhoji baada ya siku moja kupita, sasa huyo alikuwa ni nani? Akalisoma jina la mtu huyo akagundua kuwa ni Tamimu Ndungai.



    "mtoto wa Ndungai ndiyo amehusika na mauwaji ya baba yake mwenyewe kweli?" alijiuliza Roi lakini jibu lilikataa kuja kwa wakati. Akalirudia tena lile karatasi kwa lengo la kusoma tarifa nzima ya mtuhumiwa anayekusudiwa. Alikuwa na umri wa miaka ishirini na Sita urefu wa futi sita na nusu. mh! akagumia Roi. Hapa kwenye urefu palimchanganya kidogo.



    "Tamimu hana urefu huu pia hata hii picha ninamashaka nayo kidogo aliwaza akiwa bado yupo ndani ya gari usiku huo. hapana kuna kila sababu ya kughushiwa hii taarifa na kama imeghushiwa ni nani aliyefanya kazi hii ya kughushi hizi taatirifa. Huyu ni mjuvi na atakuwa yupo ndani ya jeshi la polisi. Usaliti ndani ya jeshi upo, hapana nahitaji kujua hii taarifa kwa undani zaidi ngoja nifanye kitu, Alichukua kompyuta yake ndogo na kuifungua akachomeka flashi ndogo aliyokuwa amepewa na IGP, alitaka kujua nini kilichopo ndani ya flashi ile. alipotazama kwa umakini akagundua alama za vidole ambazo zilipatikana kwenye kisu kilichotumika kumuulia Ndungai. Hakupoteza muda akajua tu fika IGP alikuwa analifahamu hili na ndiyo maana ameweza kumpa hivyo vitu viwili kwa wakati mmoja. Hakuchelewa Roi, alichokifanya ni kuzitituma mahali picha zile alipohakikisha zimekwenda, aliizima kompyuta yake na kutoweka. Alikuja kutokea kwenye Kasino kubwa la matajiri ambao hufanya unyang'anyi wa mali za watu kwa kutumia akili za kuzaliwa.



    Roi aliingia ndani humo akiwa na lengo moja tu nalo ni kuhakikisha kuwa anampata mmoja kati ya wale vijana waliomkamata Tereza siku iliyopita ili kuweza kumsaidia binti huyo. Taarifa alizozipata kupitia file la siri lililopo kwenye kompyuta ya binti huyo ilimpa uhakika wa kujua kuwa kuna watu watatu aliokuwa akiwatafuta na watu hao ni kwamba walikuwa ni raia wa nchi ya Malawi sasa haikujulikana ni kwanini walipofika humu ndani ya Taifa la Ungamo wawe ni watu wenye heshima kubwa tena huku huyo mmoja akitambulika kama muheshimiwa na wakati kule Malawi anasakwa kama muuwaji wa binti wa Waziri mkuu wa taifa hilo. Alikuwa amechagua sehemu ambayo ilikuwa tulivu sana. Aliagiza kinywaji kikali akawa anapiga kidogo kidogo ili kuweza kugundua windo lake litakuwa mahali gani. Mwanga hafifu wa lile eneo alilokaa, uliweza kumficha vizuri tu yeye ndiye aliyekuwa akiwasanifu wote walioko ndani mule. Mbele ya jukwaa moja kubwa aliweza kumuona binti mrembo ambaye alikuwa akikata ngoma kwa kujimwaga kabisa. Alianza akiwa amevaa vizuri kisha kila muziki ulipokuwa ukinoga ndivyo dada huyo alivyokuwa akipunguza mavazi yake yaliyopo mwilini hadi kubakiwa na nguo ya ndani pekee. Roi alijisahau kabisa kuwa alikuwa pale kwa lengo gani alichokiwaza na kukifikiri kwa wakati huo ulikuwa ni uzuri wa yule binti. Macho yake yalikuwa imara sana kuhakikisha hapotezi pointi hata moja katika utazamaji wake. Mate ya uchu yalimdondoka si utani. Wakati akiwa anazidi kushangaa hapa na pale huku mara moja jicho lake likirudi kwa yule mrembo, alijishangaa kumuona yule mrembo akitoka pale jukwaani kisha kuwa kwenye meza yake akiwa amemrembulia macho yake mazuri ya kuvutia.



    "Habari yako kaka?" alisalimia yule binti akiwa katika tabasamu pana la kuchombeza. Tabasamu ambalo hata kama ungelikuwa na mawazo kiasi gani yangehama kwa muda na kubakiwa na kitu kimoja tamaa ya ngono.



    "salama vipi mrembo!" alijibu salamu Roi akiwa kwenye tabasamu pia.



    "mmh! wewe ni kijana mtanashati sana sidhani kama ni mrembo kuzidi utanashati ulionao" aliongea huyo dada. Roi akaona huo haukua muda wa kupoteza kwani kiumbe huyo adimu ameingia mwenyewe kwenye kumi na nane za mwindaji hivyo hana budi kumrarua kama Simba.



    "napenda kuwa nawe kwa usiku wote huu ili niweze kujiona nami ni mtu kwenye watu" aliongea Roi huku akitaka kusikia itikio la mtoto huyo wakike mwenye sifa kemkem.



    "Nipo hapa kwa ajili hiyo ila sidhani kama mtu kama wewe unaruhusiwa kutoka na mimi usiku huu, unaonekana ni mgeni sana eneo hili. Nimebahatika kuona matajiri wengi sana lakini sikuwahi kukuona wewe na ni nadra sana tajiri mgeni kuingia humu bila kukaribishwa na kupimwa utajiri wake, watu wa humu ni wakorofi na ni makatili sana" alisema huyo binti, Roi akatulia kama si yeye eneo lile alionekana kuyahifadhi ubongoni mwake yale maneno yalikuwa kuntu sana. Akataka kusema kitu lakini hakuwahi, alikuja kijana mmoja aliyeonekana amelewa sana, huyu aliukamata mkono wa yule mtoto wa kike kisha kuuvuta kwa nguvu kiasi cha yule binti kutaka kudondoka. Roi alipomtazama vizuri usoni yule kijana aliikumbuka ile sura, alikuwa ni miongoni mwa wale vijana waliopewa mamlaka ya kumkamata Petii usiku uliopita.



    "shit!!" aling'aka kidogo kisha akashusha macho yake mezani ili kuzuia mshangao wake kwa watu walio makini kwani alijua fika pale alipo si salama kwake.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "nilikuambia nini...mimi, hujui...nakuuliza hivii....hujui? Mimi nilikuambia kuwa....hebu ngoja kwanza suruali inanivuka, ngoja nifunge vizuri mkanda....wewe si nilikuambia kuwa ukimaliza kucheza muziki unakwenda kulala na mimi sasa mbona uko na huyu kima hapa sijui Ngedere sijui Tumbili...huyu atakuwa ni Mbega wa Kakamega" alikuwa akiongea kilevilevi yule kijana huku akiwa amemshika yule binti mkono. Alikuwa akiyumba sana lakini hakuthubutu kumuachia hata kidogo. Roi alitingisha kichwa kusikitika mara baada ya kuona kadi ya biashara mezani kwake akajua tayari binti huyo ameweka mawasiliano yake hapo. Akatabadamu na kuitumbikiza ile kadi kwenye mfuko wa nyuma wa suruali yake hakutaka kuipoteza. Alipiga gilasi moja ya pombe ile aliyokuwa ameiweka juu ya ile meza kisha akamimina nyinge lakini kabla hata hajaimimina tumboni mwake, akatupa jicho kule ambako yule jamaa na yule binti walikuwako. Macho yake yalishuhudia yule kijana akiwa amemuacha yule binti kwenye kiti fulani kisha yeye akiwa anayumbayumba kuelekea mahali vilipo vyoo. Roi akainama na kujisemea kuwa sasa windo lake liko kwenye mtego wa Nguruwe pori lazima aimbe nalo. Akapiga funda kubwa huku akimshuhudia yule bwana akikunja kona kuelekea chooni. Naye akajinyanyua vivo hivyo kilevi, akawa anapiga hatua mbele moja nyuma kidogo au mbele mbili nyuma kidogo hali iliyopelekea kufika chooni kwa haraka sana. Alikuta mlango mmoja wa chooni ukiwa wazi alijiingiza kwenye huo huo mlango akamkuta huyo kijana akiwa anafurahi starehe ya haja yake ndogo jinsi inavyotoka kwa utamu. Alikuwa amefumba macho kabisa huku matusi na mashuzi yakimtoka.



    "Yule malaya....bado anateseka kweli au mkuu amemuachia?" aliamua kutupa karata yake Roi ya kupima kama anaweza kufanikiwa kwa kuamua kumuuliza huyo kijana kuhusiana na Petii.



    "Yule malaya hawezi kupona hata....hata kidogo" akabeuwa kisha akaendelea tena.



    "Mkuu amemfungulia baridi kali sana Hivi punde tu. hapa hadi kesho atakuwa maiti na atakuwa ameganda sana. Ice room siyo chumba cha mchezo mchezo kabisa" alijibu kilevi yule kijana kiasi cha kumpa nafasi nzuri Roi ya kujua kumbe kama angeendelea kuzembea basi Petii asingekuwa hai tena.



    "hiyo Ice Room iko floow ipi maana aagh....!" naye akabeua Roi kuonesha kuwa kilevi kilikuwa kimemkubali vilevile.



    "wewe nawe ni mat*ko sana...unakaa ndani humu unasahau chumba cha barafu....si floow namba mbili ground" alijibu huyo kijana huku akionekana kukung'uta zakari yake baada ya kuwa amemaliza kuitendea haki haja ndogo hiyo.



    "Asnte sana kwa kunisaidia" alijibu Roi hali iliyopelekea huyo kijana kushtuka inawezekana vipi muda mfupi uliopita aweke sauti ya kilevi na hapo aoneshe kuwa ni mkavu na hakuwa amelewa kabisa. Kitendo hicho kikamfanya huyo kijana kujua huyo hakuwa mwenzake na tayari alikuwa ameuuza mchezo. Akarusha ngumi mbili nzito za haraka lakini hazikuwa zimezaa matunda, Roi alihama kidogo na kumzawadi huyo jamaa 'Palm vibrate' ya tumbo, jamaa akataka kutapika pombe aliyokunywa, Roi akamwambia si vema kujitia hasara kwa kunywa kwa gharama kisha aitapike. Pigo moja maridadi likakita kwenye koromeo jamaa akaguna mh! Kisha kumaliziwa na pigo moja baya sana la chembe ya moyo, huyo bwege badala ya kutapika pombe, sasa akawa anatapika damu huku akishuka chini kwa kuinama. Pigo jingine zito lililopigwa kwa ufundi mkubwa nyuma ya shingo lilikwenda kuvunja kabisa pingili moja ya mshipa huo. Bwege huyo akashuka chini kwa kishindo akiwa ni marehemu tayari. Akatoka mule ndani ya choo akiwa ameuficha ule mwili mahali salama kabisa ambapo ni vigumu sana kuweza kuonekana kirahisi. Alitazama muda ilikuwa tayari ni saa sita akajua kwa vyovyote vile hali ya Petii kwa muda huo itakuwa mbaya kabisa. Akazunguuka kwa upande mwingine ambako kulikuwa na mlango mdogo huko alikutana na mlinzi mmoja ambaye hakutaka kumkawiza, alipomkaribia tu mlizi huyo alimpiga kwa mapigo matakatifu yaliyompotezea uhai bila kuomba maji. Aliuchukua mwili wa mlinzi huyo kisha akusogeza kizani. Baada ya dakika moja, Roi alitoka hapo kizani akiwa yupo ndani ya yale mavazi ya yule mlinzi, alizama moja kwa moja ndani na ilikuwa ni kwa haraka kubwa na umakini wa hali ya juu sana kwani hakutaka kutambulika mapema pia aliamini kujulikana kwake ni wazi asingeweza kutoka ndani ya ile Kasino. Alitakiwa kutoka kabla hawajagundua miili ya maiti mbili alizoziuwa. Alifika hadi flow ya pili ground ambayo aliambiwa kuwa huko ndiko Petii alikohifadhiwa. Hakupata shida kuona chumba kidogo kilichokuwa kimeandikwa Ice Room, aliingia ndani ya chumba hicho kwa kutumia funguo zake za bandia ambazo hazijawahi kushindwa na kufuli la aina yoyote ile. Alipofungua tu mlango wa hicho chumba cha baridi, alikumbana na baridi kali sana iliyokuwa ikipuliza humo ndani. Alitukana tusi zito sana kwenda kwa wamiliki wa jingo hilo kisha akamsogelea Petii aliyekuwa ametulia tuli huku zilizokuwa zimemzuia mahali hapo ni kamba alizofungiwa pekee. Alimfungua zile kamba kisha akamvisha lile gwanda la mlinzi alilokuwa amempora mlinzi huko nje akachukua mkanda mgumu sana uliopo kiunoni mwake akamuweka Petii mgongoni kisha akambana vizuri na ule mkanda. Alipohakikisha amemfunga vizuri, alitoka nae mule ndani mkononi mwake akiwa amekamatia bastola. Alipofika kwenye ile korido ndefu, akasikia king'ora cha hatari kikilia akajua hao jama wameshamuona na wamejua kuwa si miongoni mwao. Roi alianza kukimbia kwa kasi kubwa huku akiwa makini zaidi. Kila aliyekuwa akijitokeza mbele yake alikuwa akikutana na risasi hakuwa na muda wa kukuna nazi mahali hapo. Alizielekea ngazi zilizokuwa zikipanda juu, kwa kasi ileile, alikuwa akiwadondosha watu vibaya sana, bastola yake ilipokwisha risasi alichomeka kibebea risasi kingine na kuzidi kufanya vitu ambavyo vilikuwa vya kutisha sana. Alipofika floow ya kwanza kabla ya kushuka huko ground, ambayo ilikuwa iko usawa wa ardhi, alikitazama kioo kilichopo mbele yake na kuanza kukimwagia rasasi huku akigeuka nyuma mara kadhaa kwa ajili ya kutoa haki hata kwa walioko nyuma. Kioo kilichopo mbele yake kilikuwa si kioo tena kilikuwa kimechanguka vibaya sana na kuacha njia. Alipenya hapo kwa kasi hadi nje ya lile jingo kisha kukimbilia kwenye maegesho ya magari. Alipotaka kuingia kwenye gari yake iliyopo hapo, alikoswa na risasi moja ambayo ilifumua kioo cha hapo mlangoni, aliliacha hilo gari na kukimbilia pikipiki kubwa lililokuwa mahali hapo kisha kuliwasha na kuondoka nalo kwa kasi kubwa mno. Risasi nyingi zilipigwa nyuma yake lakini hakutaka kuzipa shabaha hata moja zote zilipiga kando kutokana na mwendo aliokua akiondoka nao na stail ya kuyumbayumba aliyokuwa akiitumia. Wakati anaingia barabara kuu, mbele yake kulikuwa na mtu naye alikuwa akija kwa kasi kubwa mtu huyo alimuwashia Roi taa kali sana kisha kuizima kwa haraka na kupishana kwa kasi kubwa. Hakuwa na muda wa kujiuliza kuwa huyo ni nani alichojali kwa wakati huo ilikuwa ni kuokoa maisha ya Petii.



    Usiku kucha Roi hakupata usingizi alikuwa na kazi ya kuhakikisha lazima Petii arudi katika hali yake ya kawaida. Alikuwa amekivuta kitanda katikati ndani ya chumba cha hoteli aliyofikia kisha kuwasha mishumaa mingi mikubwa kuzunguka kitanda kile, akamfunika na shuka zito sana ambalo aliamini ni lazima litaweza kuzalisha joto kwa haraka sana. Petii alikuwa katika hali mbaya na ya kuogopesha japo alikuwa akipumua lakini alikuwa amepasuka papi za midomo yake, alikuwa amepauka sana kutokana na baridi kali ya chumba kile. Hali hiyo aliamini kama hatakuwa makini, inaweza kumletea matatizo baadae binti huyo. Alipohakikisha kuwa amefanya ya kufaa akajilaza pembeni ya kitanda hicho na kumkumbatia kwa ajili ya kumuongezea joto huku akitafakari hili na lie.



    Asubuhi kulipokucha Petii alijishangaa sana kujiona yu katika shuka zito na kitanda safi chenye kuleta raha huku akiwa amekumbatiwa. Alikurupuka. Mwili ulikuwa ukiimuuma sana lakini hilo halikuwa lenye kumuumiza sana kwani maumivu yalikuwa ndiyo sehemu ya maisha yake. Alishangaa zaidi alipoona mishumaa ikiwa inamalizikia, hofu ikaanza kumkumba, neno nimeingiliwa kimwili pasipo ridhaa yangu likawa la kwanza kumjia lakini alipotazama pembeni akamuona kijana akiwa amelala tena akiwa hana fulana bali ni suruali tu na muda mfupi alikuwa amemkumbatia. Akataka kusema Mungu wangu nimebakwa lakini midomo ikamuuma akabaki kuisema kauli hiyo moyoni. Akalifunua lile jishuka zito akastaajabu kujiona na gwanda linalotumiwa na walinzi wa sehemu aliyokuwa ametekwa, alipotazama vizuri, akajikuta na vazi lake lile lile haikutosha, akapeleka mkono kunako huko akashusha pumzi nzito sana baada ya kujigundua kuwa yuko salama. Akageuka tena kumtazama huyo kijana akakutana na tabasamu zito huku likisindikizwa na sauti nzito ya asubuhi.



    "Woga umekujaa sana mrembo, ulidhani nimefanya vitu visivyoendana na ubinadamu...nimefurahi sana kwa kuwa umerudi tena duniani, pole kwa yale yote yaliyokukuta kwani ni moja ya sehemu ya maisha uliyoyachagua" alisema Roi. Petii hakuweza kuongea chochote alibaki kuongeza tabasamu kwani alimkumbuka vizuri sana huyo kijana kuwa ni yule aliyemsaidia Tamimu kuingia katika ushindi wa Kampuni yake ya magari kupata nafasi ya kuingia kimataifa kibiashara, pia alikumbuka kuwa huyo ndiye yule aliyemlipia bili ya chakula hivyo aliamini kwa asilimia zote hapo alipo ni salama kabisa. Walitazamana kwa muda huku matabasamu pekee yakiwa ndiyo yaliyochanua mahali hapo, Petii alimuona huyo kijana kuwa ndiye mkombozi wa maisha yake japo hakujua ni vipi huyo kijana aliweza kugundua uwepo wake ndani ya lile jumba ambalo kama si kudra za mwenyezi Mungu basi ingekuwa ni historia nyingine ya maisha yake.

    "ni vema uamke sasa maana muda umekwenda mno, nataka kujua mengi kutoka kwako" aliongea Roi huku akimuangalia huyo dada moja kwa moja usoni. Petii alijichungulia tena kisha akalivuta lile shuka pembeni akaiteremsha miguu yake taratibu.



    "hebu jaribu kusimama" akasema Roi, Petii akasimama taratibu alikuwa akihisi maumivu kwa mbali kidogo lakini hakutaka kuyajali, alijikaza. Petii alikuwa ni mrembo sana, umbo lake lilikuwa si umbo la kulitazama kwa macho tu ukaridhika, lilikuwa ni umbo lenye kuamsha hisia za ndani za kimatamanio. Kijana Roi alijikaza kisabuni lakini hakuweza kuificha hali hiyo mbele ya binti huyo mrembo wa kimalawi. Mapaja yake manene ya rangi ya Chokoleti yenye kunyurutika yalikuwa yakimpa ashki kijana huyo.



    "kunywa hizi dawa kisha haya mafuta utapaka kwenye papi za midomo yako ili kuweza kuiweka ngozi yako sawa, baridi ilikutafuna sana na kwa hali niliyokukuta nayo sikutegemea kama ungeweza kuwa hivi hadi sasa" alisema Roi. Petii alijitahidi kunyanyua kinywa chake na kusema kuwa, hana zaidi ya zawadi ya kuweza kumpa kijana huyo zaidi ya asante, alimshukuru sana Roi kwani kwa hali ilivyo mule ndani ya kile chumba alikuwa si wa kutoka mule akiwa hai. Alikumbuka baadhi ya mifupa na mafuvu aliyoyaona mule, damu zilimsisimka sana na hakuweza kuamini. Roi alimshika mabega huyo binti kisha akamtazama usoni kwa muda kidogo, alimtazama kwa namna yake sana hadi Petii akaona aibu kuendelea kumtazama kijana huyo.



    "Chakula utakuwa ukiletewa kila baada ya kuda husika, unatakiwa ule ili afya yako itengemae, hakikisha unakula kwa wakati. Mimi nawe tutaonana jioni" alisema Roi kisha akatoka humo ndani akiwa anamuacha huyo binti akiwa anamtazama kwa macho ya huruma.



    "Pumbavu!! Nani wa kuweza kuharibu kile kitu nimepanga mimi, nani nasema huyo asiyekiogopa kifo chake?" alifoka Bande Sir akiwa kwenye kiti chake cha kiofisi, alikuwa bado yupo kwenye moja ya ofisi yake ya kazi kama waziri. Simu aliyopigiwa ya kumueleza uharibifu uliotokea ilikuwa imemchanganya sana asubuhi hiyo.



    "Bob unasema kuwa huyo mtu alikuwa ni mweusi au mweupe?" aliuliza Bande Sir akiwa amesawijika kwa hasira.



    "Ni mweusi mkuu na ni hatari sana kwani tukio hilo amelifanya ndani ya dakika tano tu lakini madhara aliyoyaacha ni makubwa sana" alijibu mtu huyo aliyefahamika kwa jina la Bob.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Nakuja muda huu" alisema Bande Sir. Akatoka humo ofisini bila ya kuaga mtu yeyote wala kuacha maagizo yoyote yale, alielekea moja kwa moja kwenye maegesho ya magari akaingia kwenye gari yake kisha akapotelea barabarani kwa kasi kubwa. Dakika takribani kumi na tano zilitosha kumfikisha bwana huyo kwenye kasino ambalo wao kwa upande mwingine waliligeuza jumba hilo ni sehemu ya kufanyia mambo hayo ya kiharamia. Kasi aliyoingia nayo ndani ya hilo jingo ilikuwa si ya kawaida hata kidogo, alionesha kuchanganyikiwa sana na hakuamini kama ipo siku ingekuja kutokea kiumbe ambaye angekuja kuichanganya akili yake namna hiyo. Alioneshwa vijana waliouwawa, walikuwa wengi sana kiasi cha kuhisi kwamba aliyefanya hilo tukio hakuwa binadamu wa kawaida.



    "Bob unauhakika huyu alikuwa mtu na umeshuhudia kwa macho yako?" aliuliza Bande Sir alipokuwa amesimama eneo ambalo Roi alilitumia kutorokea.



    "kwa picha niliyoiona kwenye camera za ulinzi, zinaonesha kuwa huyu ni mtu na wala si vinginevyo" alijibu Bob.



    "nataka kumuona kupitia hiyo picha yake" alisema kisha wakatoka hapo hadi kwenye chumba kinachotumika kuongozea hizo kamera, kitu alichokiona kilimfanya atulie kwanza kidogo kwani kasi aliyokuwa akiitumia mtu huyo ilikuwa si ndogo hata kidogo. Akakubaliana na matukio yale ya mauwaji lakini hakutaka kukaa kimya bila kutoa taarifa kwa mkuu wake wa kazi. Hivyo aliagiza aunganishwe na Mh. Julio muda huo huo. Simu ikaunganishwa kisha kukabidhiwa. Akapeleka hizo taarifa ambazo zilikuwa mpya kidogo kwa kigogo huyo wa zamani ikabidi wote wawili wabaki wakijiuliza ni nani huyo aliyefanya hayo mambo. Jibu hakuna hata mmoja aliyekuwa nalo kwani kila mmoja hapo alikuwa hajui na hata video zilizopatikana kwenye CCTV, hazikubahatika kuiona sura ya mtu huyo. Kikao cha haraka kikaitwa na vigogo hao wawili ambao walikwenda kukutana kwenye jumba kubwa la Mh. Julio Mobande, wakateta.



    "Inabidi kuwa macho kuanzia sasa, tuhakikishe kona zote sasa zinafungwa hii yaweza kuwa hatari kwetu na utakuwa ni uzembe mkubwa sana. Nimepokea taarifa kuwa huko Madagascar mambo yanakwenda kukamilika ya kukamilisha huu mpango wa sisi kuwa madarakani na kufanikiwa kuiweka chini yetu hii nchi maana dawa ya kuwaangamiza wale wote vimbelembele wa taifa hili imeanza kutengenezwa. Sitegemei kuona hili tena likitokea" aliunguruma Julio kisha akamgeukia Bande Sir na kumwambia, sasa huo ndiyo ulikuwa muda wa kuhakikisha wanamtafuta huyo Nguchiro popote pale lilipo shimo lake kisha auwawe yeye na mayai yake ili wasiwe na wasiwasi tena. Kikao hicho kikaisha watu wakatawanyika huku Bande Sir akiwa ameshapanga watu wake wa kazi kila mahali. Julio yeye alikuwa bado akihitaji kujua ni wapi yule kichaa alipokimbilia kisha auwawe kwani kuwepo hai kwa kichaa huyo, kwake ilikuwa ni hatari kubwa kuliko hatari ilivyo. Kitema akaahidi kuwa muda si mrefu huyo kiumbe angeileta roho yake hapo kisha yeye kuamua kuipeleka peponi au kuzimu.



    Jiji la pande lilikuwa limepoa sana kanakwambwa kulikuwa hakuna pilikapilika zilizokuwa zikiendelea. Watu walikuwa wakifanya yao huku wakiwa wamesahau yale matukio ya kutisha yaliyokuwa yametokea katika hospitali kubwa ya jiji hilo lakini kumbe wakati wakiwa wao wamelipotezea hilo kuna watu walikuwa wakitaka kujua ni sumu ya aina gani iliyofanya yale. Ile miili ya wapelelezi iliyokuwa imepelekwa Tanzania kwa ajili ya kufanyiwa mazishi ndiyo iliyokuwa imebeba na baadhi ya mifupa ambayo ilitakiwa kwenda kufanyiwa uchunguzi maalum. Miili ile ilikuwa imebeba siri ile ambayo ni wachache tu ambao ndiyo walikuwa wakifahamu hilo, naye ni Rais Mabandu na IGP pekee.



    DAR ES SALAAM TANZANIA.

    Madaktari maalumu walikuwa ndani ya maabara maalumu iliyotengwa kwa uchunguzi maalumu ndani ya hospitali kuu ya Muhimbili. Alikuwapo Dr. Lyimo pamoja na wasaidizi wake wakiwa wanaendelea kuifanyia uchunguzi mifupa ambayo imetoka ungamo. Hii ni ile ya askari ambao walikufa kifo cha ajabu sana, kifo cha kuvuja damu nyingi baada ya kudhuriwa na silaha yenye kemikaki mbaya sana kisha baadae kuoza ngozi zao za mwili bila kutoa harufu yoyote na kupotea kabisa kisha kubaki mifupa mitupu. Madaktari hao walikuwa wametengeneza kemikali kadhaa ambazo walizihifadhi kwenye Tube mbili, kemikali moja ikiwa na rangi nyekundu lakini nyingine ikiwa na rangi ya kibuluu kisha kuchukua kipande cha mfupa wakakiweka kwenye chombo kidogo sana cha pembeni. Wakachukua kemikali ya kwanza wakamimina kidogo kisha wakachukua na ya pili ya kibuluu nayo wakaichanganya kidogo sana. Wakatulia kwa dakika moja nzima, wakautoa ule mfupa ambao ulikuwa umelika upande ambao ile kemikali iliishia, wakaugonga kidogo kwenye chombo kikavu kabisa wakakitumbukiza hicho chombo kwenye mtambo mdogo ambao ulianza kusoma taratibu.



    "Kompyuta imetoa alarm, tazama ni kitu gani kimesoma huko" aliagiza Dr. Lyimo baada ya kompyuta kutoa alarm kuonesha kuwa kunakitu kilianza kuonekana huko.



    "Unaweza kuja kuona Dokta" alisema daktari mmoja ambaye alikuwa akifuatilia kile kitu kilichokuwa kikirushwa kwenye ile kompyuta baada ya kusomwa kule kwenye kile kimashine.



    "Aisee! Ni silaha ya kibaolojia hii, sasa kwanini hawa watu wametengeneza hii na walikuwa na mpango gani kwa maisha ya watu. Ni sumu moja hatari sana hii na asili yake ni huko nchini Urusi. Sumu hii Hutoka kwenye madini ya Zinc kisha kuchanganywa na kemikali ambazo hudadavuliwa kutoka kwenye baadhi ya wadudu wenye sumu za kuleta madhara kama N'ge, Buibui na Tandu. Sumu hiyo kutoka kwenye hayo madini ambayo imepewa jina fupi tu la ZIC, inapochanganywa na sumu kutoka kwa hao wadudu na baadhi ya kemikali, huwa ni sumu mbaya na yenye madhara makubwa mno" alisema kwa kina kidogo Dr. Lyimo akiwa mbele ya wasaidizi wake makini na anaowaamini.



    "Ulijuaje yote haya dokta" aliuliza msaidizi mmoja.



    "lazima nijue haya kwani baada ya kuweza kuigundua hii kemikali ndiyo nikakumbuka kuwa hii ndiyo kemikali pekee iliyofanikisha kumtorosha gaidi mmoja ambaye hadi leo hajulikani alipo. Gaidi hili lilikuwa limeingia Tanzania tena ndani ya jiji la Tanga kwa mpango maalumu wa siri sana. Huyu bwana alikuwa ni katili na muuwaji wa siri ambaye hutumiwa kuuwa tu. Matajiri wengi wakubwa walikuwa wakimtumia huyo bwana kwa ajili ya kuuwa ili kuweza kufanikisha mambo yao sasa kuna Bilionea mmoja wa kirusi alikuwa akimuhitaji huyo Muuwaji ndipo akamtumia hiyo silaha ya kibaolojia kwa siri sana na ilipakwa kidogo sana kwenye kijichupa kidogo cha dawa ya PPF. Gaidi hilo likafanikiwa kuwaangamiza walinzi wote wa usiku kwa hiyo silaha kisha likapotea. Mimi ndiye niliyepewa kazi hiyo ya kuichunguza miili ya askari wale wote waliouwawa kinyama, ndipo nikagundu waliuwawa kwa sumu hiyo. Na ukitaka kujua vizuri huo mkanda kwa urefu na umakini zaidi, fuatilia DEREVA TAX II (na harakati za kigaidi). Mkasa huo makini na wa hatari uliopoteza roho za watanzania wengi umeandikwa na mwandishi wa watu Ahmed Jiriwa." alijibu kwa urefu tena Dr.Lyimo. Mara mlango wa hicho chumba ukafunguliwa, akaingia mzee mmoja ambaye alikuwa ndani ya mavazi ya kidaktari yaliyokuwa yamemkaa vizuri, machoni alikuwa na mawani safi ya macho.



    "vipi uchunguzi umekwenda vizuri?" aliuliza huyo mzee huku akiwatazama hao madaktari kila mmoja kwa nafasi yake.



    "bila shida Babu na kila kitu kipo ndani ya hiyo karatasi hapo mezani" alijibu Dr. Lyimo kisha kuichukua karatasi na kumkabidhi huyo mzee aliyekwenda kwa jina la Hussein Babu au D.A kama wengi walivyokuwa wakimfahamu. Babu aliichukua hiyo karatasi akaiweka kwenye bahasha ya khaki na kuitumbukiza kwenye kibegi chake kidogo cha mkononi akatoka humo ndani baada ya kutoa shukurani kwa hao vijana. Alipotoka nje ilikuwa ni moja kwa moja kwenye gari yake ambayo mara nyingi huwa akiitumia akiwamo ndani ya jiji hilo la shida na raha. Aliitazama saa yake ya mkononi ikamwambia kuwa kwa muda huo ilikuwa imetimu saa kumi za jioni.



    "kazi ilikuwa si ndogo heko kwa vijana wale" alijisemea Babu baada ya kulitupia lile begi kwenye kiti cha pembeni akawasha gari yake taratibu akaondoka katika viunga hivyo vya hospitali ya Taifa Muhimbili akielekea uwanja wa ndege kisha arudi zake Morogoro zilipo ofisi zao za siri.



    PEMBEZONI MWA MAPOROMOKO YA MTO ZIGI.

    Kichaa M.Y.S alikuwa ametulia juu ya jiwe moja akiwa anayatazama maji jinsi yanavyotiririka kwa mtindo wa pekee na wa kuvutia sana. Macho yake hayakuwa yakipepesa hata kidogo, alikuwa akitabasamu kila wakati mithili ya mtu aliyekuwa akiona jambo la kufurahisha likipita mbele ya macho yake. Nywele zake chafu zilizojisokota kwa mtindo wa rasta, shati baya lililopoteza rangi lakini pia likiwa si lenye sifa ya kuitwa shati tena kwani lilikuwa limepasuka sana maeneo ya mgongoni huku likiwa limefungwa kwa mafundo kadhaa ili kuweza kuipitisha mikono vizuri. Suruali yake iliyokuwa imepasuka ama kufumuka kuanzia magotini kwenda chini na kuifanya kuwa 'Buga' fulani hivi. Kuna kipande cha karatasi kilikuwa mkononi mwake ambacho haikujulikana kilikuwa ni kipande cha gazeti ama laa! Lakini kadiri muda ulivyokwenda ndivyo alivyokuwa akitabasamu. Alitulia vivo hivyo kwa kama dakika tano ama sita kisha akakitazama kile kipande cha karatasi halafu akatamka jina moja tu ambalo mara nyingi sana hupenda kulitamka, jina hilo llilikuwa lipo kwa mfumo wa herufi 'J.M.J' kisha akatulia tuli na kulipoteza kabisi lile tabasamu ambalo alikuwa akilitoa mara kwa mara. Akasema.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Umenibatiza jina baya sana kisa tu niliona unyama wako uliowahi kuufanya zamani, Unyama ambao ulinifanyia mimi mwenyewe kwa ujinga wako usio na mantiki, hukujali kuwa nilikuwa mtoto nisiyejua kitu, Juhudi zangu ndiyo zimeleta haya? Hivi ni kweli? Hukujali kuwa nilikuwa na ndoto kubwa za kuja kuwa mtu mkubwa na mwenye heshima kama uliyokuwa nayo wewe" akameza mate na kuyashangaa mawingu kisha akaendelea.



    "Wazazi wangu, wazazi wangu, kwanini sasa? Kwanini uliamua kuwahukumu wazazi wangu kwa sababu yangu? Hivi unadhani nitasahau kifo alichokufa baba? Unadhani nitakuwa sawa nikikuacha wakati ulimuuwa mama yangu kwa maumivu makali kisa alikataa kukuonesha nilipo. Raisi, watu walikuwa wakikuheshimu na kukuthamini kumbe ulikuwa katili usiyejali maisha ya yule unayemuulia wazazi wake pindi atakapobakia mwenyewe" akafumba macho kwa hasira sana M.Y.S, chozi la uchungu likamdondoka, akachelewa kulidaka na kuliacha lidondoke chini kwa kishindo cha uzito wake. Alipokuja kuyafumbua, Tayari machozi yalishajaa kwenye mashavu yake. Alikuwa akilia kwa uchungu sana kijana huyo, aliwaza mengi akilini mwake na mengi yalipita kichwani mwake lakini hili katu haliwezi kufutika ilikuwa ni lazima alikumbuke. Juu ya jiwe kubwa alilokuwa amesimama huku macho yake pekee yakitalii hiki na kile, Kumbukumbu mbaya na asiyopenda kuikumbuka ilimjia kichwani mwake, kumbukumbu ambayo ndiyo iliyomfanya yeye aishi maisha yale.





    *****************

    *************************

    ***********************************



    USIKU WA KAFARA.



    Giza lilikuwa limetanda kila kona ya jumba hilo hakukuwa na taa hata moja ambayo ilikuwa ikiwaka mahali hapo. Giza hilo lilikuwa ni kero kubwa kwa watu wengine ambao hawakujua nini maana hasa ya giza hilo lakini kwa watu wengine hilo wala halikuwaathiri hata kidogo. Taa zote za jumba hilo zilizimwa. Kila mtu wa jumba lile alikuwa katika mavazi ya ajabu na hakujulikana yupi ni yupi na nani ni nani, walikuwa wamevaa nguo ndefu zenye kofia zilizofunika vichwa vyao huku sura zao wakiwa wamezielekezea chini kiasi cha kufanya iwe ngumu kidogo kuwafahamu. Kimya kilikuwa kimetanda, hakuna wa kuongea kilichosikika hapo ni hatua zao ambazo walikuwa wakizipiga kwa kuburuza miguu. Safari hiyo waliyokuwa wakiitembea, ambayo ilikuwa ikiongozwa na mwanga hafifu wa muenge wa moto ulioshikwa na mtu mmoja aliyopo mbele ya msafara huo, uliishia kwenye chumba kimoja kikubwa na cha ajabu sana. Chumba hicho kilikuwa cheusi kilicho na giza la kutisha sana. Watu wale walijipanga mstari na kutengeneza umbo la herufu 'V'. Kiongozi alikuwa amekaa katikati ya ile 'V' akiwa kwenye baiskeli yake. Hakuwa mwingine bali ni Dr. Lee. Alianza kuongea maneno ya ajabu kwa sauti ya chini sana lakini kila alivyokuwa akizidi kuongea ndivyo sauti yake ilivyokuwa inazidi kuongezeka hadi kufikia kwenye ile hali yake ya kawaida. Yalikuwa ni maneno ambayo hakuna mtu mwenye kuweza kuyaelewa hata mara moja. Watu wawili tu ndiyo walikuwa wakijua hicho kilichokuwa kikizungumzwa mahali hapo. Maneno yalizidi kwa takribani masaa mawili kisha kimya kikakita tena. Kilikuwa ni kimya kizito sana. Baada ya kimya hicho, mlango wa hicho chumba ukafunguliwa, vijana wawili wakaingia ambao walikuwa wamefunika sura zao huku wakiwa wameongozana na vijana wengine wawili hawa walikuwa wamefunikwa sura zao kwa nguo ngumu na nyeusi ambazo ziliwafanya wasijue kabisa mahali walipokuwa wakipelekwa. Walipofikishwa ndani ya chumba hicho kikubwa, Merina akanyanyua shingo yake na kumtazama mkuu wake.



    "wakague wote kama wako sawa?" ilitoka kauli hiyo kwa sauti ya chini sana. Merina akawatoa nguo wale watu waliokuwa wamefunikwa usoni kisha akaagiza na wengine waletwe mahali hapo. Walipoletwa hali ilikuwa ni hiyo hiyo ya kukaguliwa kwa kutumia ule mwanga hafifu wa muenge wa moto kisha maneno ya ajabu yakaanza upya huku Lonto akitoka mbele mahali ambapo wale vijana wapo. Akatoa amri wafungwe kamba imara kabisa, amri ikatekelezwa. Akakamata Jisu kubwa na kulipitisha shingoni mwa kijana mmoja kisha akamsukuma yule kijana hadi akaangukia kwenye mtaro mmoja uliokuwapo mahali hapo kisha akakanyagiwa na miguu yenye nguvu nyingi, damu ikawa inachuruzikia kwenye ule mtaro. Hali iliyomtokea yule kijana, ikamkuta kila aliyekusudiwa hadi wote wane walipokwisha. Dr. Lee akapiga kimya kingine kizito kisha akatulia kama si yeye aliyekuwa akiongea kwa sauti yake kubwa na mbaya. Hali ya hewa mule ndani ikaanza kubadilika, harufu mbaya ya kuziba pua ikaaza kuhisiwa na kila mmoja aliyopo maeneo hayo lakini amri waliyopewa ni kwamba hawakutakiwa kufanya jammbo lolote lile zaidi ya kutulia tuli. Harufu ikazidi kuwa kali sana kiasi kwamba kama ungelikuwa na moyo mwepesi ungeweza kutapika. Harufu ile ilizidi kuzisumbua pua za kila mja aliyekuwepo mahala pale kisha muenge ule ulikuwa ukiwaka ukazima pasipo mtu yoyote kujua ni nani wa kuuzima ule muenge wa moto.



    Wakati Muenge ule ukiwa unazima, kwenye chumba cha ndani alichokuwa amelala Tereza hali ilikuwa tofauti kabisa. Tereza alianza kuhangaika pale kitandani kisha akatulia kimya baada ya kuhangaika kwa muda wa dakika kama tatu. Nafsi yake ikaamka taratibu kisha ikatoka kabisa kwenye mwili ule usioelewa kitu na kutoka kabisa ndani ya chumba kile na kuvamia chumba kilichokuwa kikifanyika kafara. Tereza alishuhudia kila kitu kilichokuwa kikiendelea na alishuhudia hadi vile ambavyo watu waliokuwepo pale walikuwa hawavioni. Tabasamu pana likakivaa kinywa chake ilihali kilichokuwa kikifanyika mahali hapo si kitu cha kumfanya mtu atabasamu. Alishuhudia mambo ya ajabu yaliyokuwa yakifanywa na kile kiumbe chenye harufu mbaya ambacho kilikuwa kikitisha mno. Kiumbe kilichokuwa kikitembea kingali kinaoza mwili, Kiumbe kilicho na roho ya ajabu sana. Hata taa ilipokuja kuwaka tayari Tereza nafsi alisharudi kwenye mwili wake. Kiumbe kile kikatoka mule chumbani kikiamini hakikuonekana na binadamu wa aina yoyote ile lakini bila kujua kuwa kuna binadamu wa ajabu na mwenye nguvu nyingi kuliko hata yeye alishamuona. Kiumbe kile kile kilipopotea kule kwenye chumba cha kafara, kilikuja kutokea kwenye chumba cha Tereza. Kumbuka kuwa hii ni mara ya pili kiumbe huyu anakuja kwenye maisha ya Tereza, mara ya kwanza ilikuwa ni kipindi Tereza ni mgonjwa akiwa hajitambui kitandani na mara ya pili ni hiyo. Ajabu ni kwamba kiumbe hicho hakikukuta mtu kitandani bali kilikuta kitanda kikiwa kitupu kabisa tena kikiwa kimetandikwa vizuri kabisa kuonesha kuwa hakikuwa kikitumiwa na mtu. Kuna kitu alikihisi mule ndani nayo ni harufu ya kiumbe kisichoeleweka. Kiumbe nyama kilicho na harufu ya kushangaza, kiumbe hicho ndicho kilichokuwa kikimkosesha amani kabisa katika akili yake. Alitafuta kwa hisia kali lakini bado hali ilikuwa ileile. Kitanda kilikuwa kitupu na kilikuwa kitupu kweli.



    Swali la kujiuliza ni kwamba Tereza alikwenda wapi? Ikiwa muda mfupi tu uliopita, mwili wake uliachwa huku nafsi yake ikitoka. Nafsi yake iliporudi kwa mara ya pili ilikwenda wapi na mwili ule uko wapi. Akili ya kile kiumbe bado haikumpa. Kila muda alikuwa akibadilika na kutisha zaidi. Mwili wake ulianza kutoa damu nyeusi damu ambayo kama utafanikiwa kuiona, ungeweza kuhisi ni sharubati ya zabibu iliyokamuliwa. Pembe yake ya juu ilianza kupotea kwa kudidimia kichwani huku damu ikizidi kumwagika kwa wingi na kuchafua sakafu ile ya pale chumbani. Pembe ile ilipopotea kabisa, macho ya kile kiumbe yakaanza kuwaka na kuleta moto wa ajabu. Sasa alianza kuitafuta harufu aliyokuwa akiihisi kwa nguvu za ajabu lakiki wapi. Harufu hiyo haikuonekana. Aliachama mdomo wake mkubwa kisha ulimi mweusi ambao ukibadilika na kuwa nyoka mkubwa wa kutisha ulitoka na kukizunguuka kile chumba kwa kasi kubwa lakini pia kitu alichokuwa akikitafuta hakikuonekana. Kiumbe kile kilipandisha hasira kali sana kikalia kwa mlio wa kutisha hakikujali kama kilikuwa ndani ya kile chumba kisha kikatoweka ghafka na kupotea mule ndani ukabaki mwangwi wa sauti yake ya kutisha. Wakati kiumbe kile kikipiga kelele, mlinzi wa karibu wa Bencov alikuwa akipita karibu na chumba hicho cha Tereza akiwa anaelekea kwenye chumba chake kwa ajili ya kwenda kujipumzisha baada ya kafara kwisha.



    *************

    ************************



    "Wazazi, wazazi wangu, kwanini sasa? Kwanini uliamua kuwahukumu wazazi wangu kwa sababu yangu? Hivi unadhani nitasahau kifo alichokufa baba? Uanadhani nitakuwa sawa nikikuacha wakati ulimuuwa mama yangu kwa maumivu makali kisa alikataa kukuonesha nilipo. Raisi, watu walikuwa wakikuheshimu na kukuthamini kumbe ulikuwa katili usiyejali maisha ya yule unayemuulia wazazi wake pindi atakapobakia mwenyewe" akafumba macho kwa hasira sana M.Y.S, chozi la uchungu likamdondoka, akachelewa kulidaka na kuliacha lidondoke chini kwa kishindo cha uzito wake. Alipokuja kuyafumbua, Tayari yalishajaa kwenye mashavu yake. Alikuwa akilia kwa uchungu sana kijana huyo, aliwaza mengi akilini mwake na mengi yalipita kichwani mwake lakini hili katu haliwezi kufutika ilikuwa ni lazima alikumbuke. Juu ya jiwe kubwa alilokuwa amesimama huku macho yake pekee yakitalii hiki na kile, Kumbukumbu mbaya na asiyopenda kuikumbuka ilimjia kichwani mwake, kumbukumbu ambayo ndiyo iliyomfanya yeye aishi maisha yale.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    KUMBUKUMBU.



    "Sioni sababu ya ninyi kuwepo hapa, mnadhani ni nani atakuwa mjinga kuwaona mkiendelea kuwepo mahali hapa ikiwa hamjalipa ada. Mtakwenda nyumbani sasa na mkifika nyumbani muwaambie wazazi wenu kuwa mkuu wa shule ametufukuza shule hadi pale siku tutukapokamilisha ada iliyokuwa ikitakiwa sawa. Wote tokeni hapa na mkawape hizo taarifa wazazi wenu muda huu" Ilikuwa ni kauli ya mkuu wa shule wa shule ya sekondari ya kata ya Mchikichini miaka kama ishirini iliyopita. Wanafunzi wote ambao walikuwa hawajalipa ada walitimuliwa shule, miongoni mwa wanafunzi hao ambao walikutwa na kadhia hiyo, alikuwa ni kijana mdogo sana mwenye nywele nyingi na nyeusi sana kichwani mwake, huyu alikuwa akifahamika kwa jina moja la Frank. Wapo wanafunzi wengi ambao hali hiyo ya kutimuliwa shule kwa kukosa kulipa ada, iliwafurahisha sana. Kelele za kuondoka eneo hilo la shule zilikuwa nyingi kiasi cha baadhi ya wanafunzi ambao wao walilipa ada, waone gere kwa kuwaona wenza wao wakiondoka shuleni hapo kwa mbwembwe. Si wote wenye akili finyu ya kushindwa kufikiri au kuumizwa na jambo fulani, miongoni mwa wajinga wawili, walikuwamo werevu wawili.



    "sina matumaini ya kurudi tena hapa rafiki yangu, kila nikiifikiria mifuko ya wazazi wangu, nashindwa kuwa na imani na masomo" alisema kijana mdogo Frank akiwa pembeni ya mwanafunzi mwenzake.



    "hapana Frank, kwanini unavunjika moyo mapema sana, darasa ulilofikia si la kuacha shule wewe. Bado mwaka mmoja tu uweze kuhitimu elimu yako sasa ni kwanini ukate tamaa?" aliongea kijana huyo mwingine aliyekuwa akifahamika kwa jina la John.



    "Si kama nakata tamaa ya kusoma Juma la! Tatizo ni kwamba deni lililosomwa hapa kuwa nadaiwa ni kubwa sana sikuwahi kujua kama tangia niingie hapa sikuwahi kulipa pesha yote, kumbe nililipiwa pesa nusu tu kama kiingilio huku nyingine wazazi wangu wakitoa ahadi kuwa watalipa kidogo kidogo lakini kumbe hadi sasa hiyo pesa haikulipwa....!"



    "Unataka kuniambia kiasi cha shilingi laki tatu zote zile zilizosomwa pale ndiyo fedha unayodaiwa?" aliuliza Juma akiwa amemkatisha Frank.



    "Haswaa! Sasa niambie kwa maisha haya ya sasa yalivyo, pesa hiyo yote wazazi wangu wataitoa wapi wakati hata pesa ya chakula ni mtihani mzito, wewe mwenyewe ukiwa shahidi rafiki yangu" aliongea kwa uchungu sana Frank, machozi yalikuwa yakitaka kumtoka lakini hakuona kama ingesaidia yeye kulia mbele ya mtoto mwenzie ambaye wote walikuwa wakitegemea msaada wa mzazi, alipigana na uchungu uliopo moyoni mwake kwa kiasi kikubwa sana japo alikuwa akiumia mno. Muda wote huo Juma alikuwa ameweka mkono wake mdomoni kwa mshangao mkubwa baada ya kufahamu kiasi cha pesa alichokuwa akidaiwa rafiki yake. Ndoto za kusoma tena zilikuwa zimeshafutika, hiyo pekee ilitosha kumaanisha kuwa Frank alikuwa tayari ameshafukuzwa shule rasmi.



    "Muamini Mungu Frank, maisha haya ni yenye makusudi sana tena yana makusudi makubwa, si maisha yenyewe ndiyo yenye makusudi kwa sisi tuishio humu bali wale wenye mamlaka ndiyo wayasababishayo haya, tumekuwa tukiishi kwa kuwaabudu wao. Najua, najua pesa hii wazazi wako wale niliokuwa nikiwafahamu mimi wasingelishindwa kulipa hii pesa. Walikuwa wakijimudu, kumbuka kuwa ulisoma kwa furaha sana ulipokuwa unaitafuta elimu ya msingi tena ulikuwa ni mwenye akili nyingi kiasi cha kuliongoza Taifa, hivi unakumbuka kuwa wewe ndiye uliongoza kwa alama za juu kabisa kuliko mwanafunzi yeyote hapa Ungamo. Hakuna mtoto wa waziri, Mbunge wala Raisi. Uliwashinda wote, watu wakabaki kuulizana, inakuwaje shule ya kishenzi kama ile tuliyokuwa tukisoma mimi na wewe, shule ambayo haikuwa na mlango maalumu uliokuwa ukitambulika, ukitaka kupitia dirishani haya, ukitaka kupitia kwenye milango isiyo na hadhi ya majina hayo pia haya. Eti ndiyo uambiwe inetoa kichwa kimoja matata sana ambacho kilikaa kileleni kuliko hata watoto wa vigogo. Hakuna wakuamini. Hapo ndipo nilipoona balaa kuhusiana na elimu yako Frank. Serikali ikalazimisha kwamba ni lazima wanafunzi tuliokuwa tukisona shule ile ya Mchikichini Primary School, tuijaze shule ya Mchikichini Secondary School, shule ambayo haikuwa imeisha majengo yake, shule ambayo ilikuwa na umasikini wa walimu na vitendea kazi. Watu wakamaka Haaaa! Hata wewe ambaye ulikuwa kinara eti, umetupwa pale? Lakini waswahili wanasema 'neno litokalo kwa mkubwa halina uvundo' inamaana ya kwamba hata kama mkubwa atakuwa ameongea vitu visivyofaaa, hawezi kupingwa kirahisi. Wanachi wakabaki na miguno lakini hakuna aliyethubutu kumpinga Rais wa Julio. Baada ya wewe kuanza shule baba yako akapewa kesi yenye mafigisufigisu, kesi isiyoeleweka na kuambiwa kuwa amekwiba mali ya ofisi aliyokuwa akifanyia kazi, kiasi cha pesa nyingi sana ziliibwa na kwa hukumu yake baba yako akafukuzwa kazi serikalini lakini pia akafilisiwa kuanzi pesa iliyopo banki, nyumba mbili alizozijenga kwa jasho lake pamoja na gari mbili za kutembelea. Akabakishiwa Nyumba moja ambyo ndiyo hiyo mnayoishi hadi sasa. Wazazi wako wakashindwa kukusomesha kuanzia pale lakini kwasababu shule ya kata ilihitaji wanafunzi wengi, wakakubali kupokea pesa nusu kutoka kwenye mikono ya baba yako mwenye uchungu na elimu yako. Sasa lile jinamizi lililoisumbua familia yako ndilo ninaloliona leo. Vumilia Frank Mungu siku zote huwa na majaribu yake na hakuna jambo alipangalo yeye mwanadamu akathubutu kupangua. Kuwa jasiri kama ulivyokuwa jasiri kipindi unanihadithia habari hii ambayo nimekuja kukukumbusha leo hii" aliongea mengi sana John, alimkumbusha mambo mengi ambayo Frank mwenyewe hakuwa akikumbuka hayo. Akaunganisha matukio hayo yote akajua kweli huwenda hiyo ilikuwa ni hujuma inayohujumiwa familia yake. Ni nani mwenye kuihujumu hiyo familia? Hapo ndipo palikuwa pagumu kujua. Akakaza moyo huku akiwa ameukamata mkono wa rafiki yake kipenzi waliotoka mbali kuanzi shule ya msingi hapo hapo Mchikichini hadi kuhamia pembeni kidogo na kuwa ni wanafunzi wa sekondari. Kidato cha tatu alikuwa akikiacha huku akiwa na maumivu makali mno lakini hakuwa na jinsi. Hapa ndipo mtu unapotakiwa kusema ile kauli waisemayo watu wengi hususani wanafunzi wengi wanapofeli. 'Kufeli shule, siyo...........!"



    Feli hii ya Frank ilikuwa si ile wanayofeli wengi, hii ilikuwa ni ya hakuna jinsi, aliyapenda masomo sana tena sana lakini hali ya kimaisha haikumruhusu kuendelea kuitumikia shule.



    "Soma sana John, ile dhamira yetu ya kwamba ni lazima tusome ili tuwe nguzo imara kwa familia zetu, naomba usiiuwe, kaza kamba za viatu na uhakikishe huishii njiani. Kila laheri. Nakuomba usinisahau, usiache kunitembelea nyumbani hata siku moja jitahidi upatapo nafasi unikumbuke, nimefeli shule John lakini katu sijafeli maisha" aliongea Frank akiwa rayari ameuachia mkono wa rafiki yake akaanza kuondoka taratiibu eneo hilo la shule ambalo labda angeweza kufika hapo kwa kumtembelelea rafiki yake lakini si kwa kuyakalia madarasa yake kwa kusoma tena, elimu yake ndiyo kwamba hapo ilifika kwenye kingo za bahari, hakuwa na matumaini ya kusoma tena labda imuangukie nyota ya jaa.



    Frank aliikata mitaa hii na ile, alipita kona moja, mbili na tatu ikiwa ni hatua ya kuhakikisha anafika nyumbani na kuwaeleza wazazi wake kuhusu kile kilichomtokea yeye na watoto kadhaa wasio na uwezo. Mawazo yalikuwa ni mengi sana kichwani mwake kila akifikiria elimu yake au safari ya kielimu kuanzia alipotoka hadi hapo ambapo ndipo eilimu ilipokuwa ikimpa mkono wa kwaheri ilihali alikuwa akiihusudu, moyo wake ulikuwa ukimuuma sana. Mwendo wake ulikuwa ni wakujisukuma bora liende lakini si kwenda kwa ubora. kila alipokuwa akikanyaga alijiona yeye tu, hata alipoifikiria dunia bado alijiona yeye pekee asiye na msaada. kwa nini? Aliwaza akiwa anajiuliza swali hilo lakini wakati akiwa anajiuliza hivyo, ile hali ya kujiona yeye pekee kwenye ulimwengu wote wa shida, ukamfanya asione kama hapo alipo alikuwa yu katika barabara ndogo inayotoka Muavengero kati kuingia barabara kubwa inayoelekea Haika. Frank alivuka pasipo kuafuata sheria za uvukaji barabara hivyo akajikuta akiwa na mashaka makubwa huku mwili ukimtetemeka, alijikuta akiwa katikati ya barabara, kelele za honi kali sambamba na sauti ya msuguano wa gurudumu za gari zilizokuwa zikisuguana na lami. Frank alijua si wa kuishi tena, hakuwa na uwezo wa kusema ajiokoe kutoka kwenye kashikashi ile, mwili wake ulikufa ganzi vibaya sana na ulikuwa ukimtetemeka sana. Gari ya gharama ilikuja kusimama umbali mdogo sana na alipo yeye. Aliyafumbua macho yake huku akishindwa kuamini. Watu walikuwa tayari wamejaa eneo hilo wakiamini kuwa tayari yule kijana wa shule amegongwa na hiyo gari. Kila mmoja alisema lake baada ya kumshuhudia kijana huyo akiwa anatweta kwa hofu aliyokuwa nayo.



    "anabahati sana huyu!"



    "Akachinje kuku wa kijani"



    "kwanza muda huu siyo wa kutoka shule ametoroka huyu, muje muwape watu kesi kwa utoro wenu usiokuwa na maana"



    "Lakini jamaa fundi sana, bado kidogo tu ampe mzinga wa maana!" zilikuwa ni kelele za kila shuhuda aliyeshuhudia alimanusura ya ajali hiyo.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "wewe mtoto wa malaya, unashangaa nini barabarani usiokwenda shule muda huu!" ikikuwa ni sauti kali iliyompa shida kijana huyo kwenye chemba ya kifua chake. Neno mtoto wa malaya lilichoma hadi ndani kabisa ya moyo wake. Nani mtoto wa malaya? Akajiuliza. Lakini wakati akiwa anajiuliza hilo, akagutushwa na kofi moja zito sana lililomtupa chini, kofi hili lilitua usoni kiasi cha kumfanya Frank kuhisi kama macho yake yalikuwa yakipasuka kwa jinsi alivyokuwa akiona 'vimemeta'.



    "Mwanaharamu mkubwa wewe, masikini wa kutupwa, ni bora hata hivyo ambavyo sijakugusa maana kama ningekugusa na hili gari ningekuharibu kabisa sura yako. Gari hili halina hadhi ya kugusa mwili wa mtoto wa kahaba kama wewe" maneno ya maudhi yalizidi kukipanda kichwa cha Frank na kukaa katikati kisha kuwaka moto wenye kumletea maumivu makali sana ya ubongo na moyo. Alipigwa teke lenye ujazo wa hali ya juu sana, teke lililopigwa na fundi anayejua wapi pa kupiga maana lilipigwa chini kidogo ya kifua. Frank alitokwa na yowe la maumivu makali mno. Kitu kama Msumari kilipenye kwenye moyo wake. Aliumia sana kijana huyo. Alinyanyua mikono kuomba msamaha lakini haikusaidia kitu, kichapo kwake kikaongezeka, sasa mpigaji hakuona tabu kumburuza kijana huyo kwenye vumbi jekundu la ene hilo huku akimshushia kipigo. Damu zilizomwagika hazikuonekana vizuri kutokana na rangi ya vumbi la eneo hilo lakini Frank alichubuka na kuumia sana. Wale watu waliokuwa wakimsema Frank vibaya sasa ile hali ikageuka, mioyo yao ikabeba ubaba na umama, uchungu wa mwana ukajenge uzio kwenye mioyo yao, huruma zikawajaa sasa wakasimama kidete kumuombea kijana huyo msamaha, ndipo alipoachiwa huru sasa lakini akiwa hawezi hata kutembea vizuri. Frank akajitahidi kumtazama yule mtu mkorofi aliyempiga kwa kipigo kile kizito, akaihifadhi sura yake vizuri, alikuwa ni kijana mrefu aliyeshupaa mwili, mwembamba na mwenye misuli iliyojitokeza kidogo, alikuwa na sura ndefu iliyokomaa. Mtu huyo akarudi garini mwake akapotea zake mitaani. Wananchi wenye huruma wakampakia Frenk kwenye baiskeli wakamfikisha mahali anapoishi. Mama na baba yake walipomuona kijana wao jinsi alivyokuwa, walilia sana, hakuna aliyeweza kunyamaza mahali hapo kwa jinsi uchungu ulivyowashika mioyoni mwao. Kijana wao wa pekee, Mtoto huyo ambaye ni kama jicho tu kwenye maisha yao. Wamepanga kumsomesha ili aje awe kioo chao cha kijitazamia, leo anafukuzwa shule. Asirudi nyumbani salama basi, anarudi nyumbani akiwa hoi vibaya sana. Baba yake akaunganisha matukio mawili tofauti kuanzia kijana huyo anafaulu kwa alama za juu kabisa kisha yeye kufukuzwa kazi na kupewa kesi ya wizi, akafilisiwa mali zake zote. Akajiminya kwa awezavyo, ampeleke shule kwa gharama kidogo na jingine liwe deni, Frank anafika kidato kimoja mbele kumaliza, amri nzito kutoka kwa Rais inasema wote wenye madeni ya kutokuwalipia watoto wao ada wafukuzwe shule hadi pale wazazi wao watakapolipa. Kisingizio eti, Taifa halina uwezo wa kuwasomesha wanafunzi wengi kutokana na kuwa chini kuichumi. Huu si mkono wa mtu kweli? aliwaza baba wa Frank, mzee Thomas. Alipoona hana uhakika na jibu lake akaamua kuachana na mawazo hayo, alimshukuru Mungu na kuzidi kumuomba biashara zake zitengemae ili asishindwe kuilisha familia. Mama yake na Frank akapasha maji ya moto kisha kuanza kumkanda kijana wake zile sehemu ambazo zilikuwa na uvimbe huku akijaribu kuyaosha majeraha yote yaliyokuwa yamejenga makazi ya lazima kwenye mwili wa kijana huyo. Hakukuwa na hospitali wala kiliniki, Frank alipona kwa mapenzi ya aliyempa mamlaka ya kuishi duniani.



    Siku zikaenda, Frank akawa amepona kabisa, kwakuwa biashara ya baba yake aliijua vizuri hivyo akaomba ajiunge na mzee wake huyo ili aweze kumsaidi angalau siku ziende lakini si kukaa nyumbani bure. Mzee Thomas akafikiria kwa kina akaona si vibaya kumvuta kijana wake kwenye biashara hiyo aliyonayo ya usambazaji magazeti kwenye majumba makubwa ya watu maarufu na hata wafanya kazi wa serikalini huku akitegemea malipo kwa mwezi ambayo hayakulipwa kwa wakati na kwa utaratibu. Frank akamwambia baba yake awe anakaa tu kibandani kisha yeye ndiyo awe msambazaji mkubwa wa biashara hiyo kwenye sehemu zote ambazo alikuwa akisambaza baba yake. Lakini wakati yeye akiwa anapanga lake, kuna watu wengine nao walikuwa wakipongezana kwa hatua walizopiga za kuhakikisha kijana yule hafiki mahali popote kwani kitendo cha yeye kufaulu na kuwa namba moja ndani ya Taifa zima wakati kulikuwa na watoto wa wakubwa ambao walikuwa wakisoma shule kubwa na zenye uwezo mkubwa na hawakupata alama hizo, ilikuwa ni aibu kubwa sana, kijana huyo alikuwa na uwezo gani kwani hadi kuwa kinara kwa Taifa zima. Haiwezekani. Likawa ndilo pingamizi la kwanza kabisa.







    Siku zikaenda, Frank akawa amepona kabisa, kwakuwa biashara ya baba yake aliijua vizuri hivyo akaomba ajiunge na mzee wake huyo ili aweze kumsaidi angalau siku ziende lakini si kukaa nyumbani bure. Mzee Thomas akafikiria kwa kina akaona si vibaya kumvuta kijana wake kwenye biashara hiyo aliyonayo ya usambazaji magazeti kwenye majumba makubwa ya watu maarufu na hata wafanya kazi wa serikalini huku akitegemea malipo kwa mwezi ambayo hayakulipwa kwa wakati na kwa utaratibu. Frank akamwambia baba yake awe anakaa tu kibandani kisha yeye ndiyo awe msambazaji mkubwa wa biashara hiyo kwenye sehemu zote ambazo alikuwa akisambaza baba yake. Lakini wakati yeye akiwa anapanga lake, kuna watu wengine nao walikuwa wakipongezana kwa hatua walizopiga za kuhakikisha kijana yule hafiki mahali popote kwani kitendo cha yeye kufaulu na kuwa namba moja ndani ya Taifa zima wakati kulikuwa na watoto wa wakubwa ambao walikuwa wakisoma shule kubwa na zenye uwezo mkubwa na hawakupata alama hizo, ilikuwa ni aibu kubwa sana, kijana huyo alikuwa na uwezo gani kwani hadi kuwa kinara kwa Taifa zima. Haiwezekani. Likawa ndilo pingamizi la kwanza kabisa.

    SONGA NAYO....



    "Nimeshuhudia kwa macho yangu akitokea shule kurudi nyumbani, anaonekana ni kijana wa tofauti sana na vijana wengine kwani wakati wenzake wakiwa wanafurahia kufuzwa shule kurudi nyumbani, yeye alikuwa ni mwingi wa mawazo makubwa kiasi cha kutembea barabarani pasipo kuzingatia sheria za barabara" ndivyo alivyokuwa akisema kijana Kitema kipindi alipokuwa amemsababishia maumivu makali Frank alipokosakosa kumgonga kwa gari yake.



    "Ilibakia kidogo tu, ningemgonga na gari kama si kutumia uwezo nilionao" alimalizia kueleza mahali hapo. Alikuwa mbele ya bwana mmoja mnene mwenye mashavu makubwa kiasi na shingo nene. Alikuwa ni Mh. Julio Mobande Alikuwa ndiye Rais wa Taifa hilo la ungamo kwa kipindi hicho.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Kwanini hukumuulia mbali?" aliuliza Rais huyo huku akiwa anamtazama kijana huyo ambaye ndiye aliyekuwa mlinzi wake wa pekee aliyekuwa akimuheshimu sana.



    "Sikuona sababu za kufanya hivyo kwa haraka, ngoja tuone kichwa chake kitafikiria nini" alijibu Kitema kisha Raisi Julio akakubaliana na jambo hilo kuwa ngoja wamuone huyo kijana kitu ambacho anaweza kufanya. Walikuwa na lengo la kuhakikisha nyota ya huyo kijana inafifia na kupotea kabisa ndani ya Taifa hilo. Mobande alikuwa na binti yake aliyekuwa amefeli vibaya sana kipindi ambacho Kijana huyo anakuwa kinara kwa Taifa tena kutokea kwenye shule ya gharama yachini mno iliyopitiwa na huruma za kiserikali ili kila raia apate kusoma kufuta ujinga lakini kumbe kulikuwa kuna watoto ambao walijua kuzitumia nafasi hasa pale wazipatapo. Hii ikawa ni aibu kwa Muheshimiwa huyo kufelisha wa kwake huku wa masikini akiwa juu. Akawaza na kufikiri akajua kuwa watu kama huyo kijana ndiwo watakao ifuta ndoto yake ya kulifanya Taifa hilo kuwa ni lenye kuongozwa na damu yake kwani wasomi kama hao baadae aliamini ndiyo watakao kuwa kikwazo. Akaamua kuwamaliza nguvu huku huku chini. Huyu ndiye aliyefanya ajualo hadi baba yake Frank kufukuzwa kazi kisha kumpa kesi iliyopelekea kufilisiwa mali zake ili tu ashindwe kumsomesha kijana wake. Alipoona bado kijana huyo anasoma kwa gharama ya serikali tena huku akiwa na deni bado, wakatoa hiyo amri ambayo kwa mzee Thomas ilikuwa ni mwiba mkali sana.



    Biashara ya magazeti ikazidi kupanda chati, ikawa si kwa nyumba chache tena bali ni kwa nyumba nyingi zaidi. Biashara ikawa inalipa kutokana na Frank kusimama kidete na kuwalazimisha wadiolipa walipe. Biashara ikatoka kwenye u-deiwaka ikawa ni mali yao wenyewe, yaani walikuwa wanachukua oda kubwa ya Magazeti na kuyasambaza kila kona ya mji huo. Mji mzima Muavengero ukawa chini ya huyo mzee na kijana wake huku kijana huyo akiwa na ndoto za kurudi shule pale mtaji utakapo kuwa mkubwa kisha kuanzisha biashara nyingine kubwa zaidi.



    "Kiukweli ni jambo la kumshukuru Mungu sana John, biashara hii imekuwa kubwa sana yote haya ni mashauri yangu kwa baba, nilimshauri jinsi ya kufanya na kweli akanisikiliza, tukafanya kitu kikubwa kabisa pasipo kuamini" Frank alikuwa akimwambia kijana mwenzake John ambaye ndiye rafiki yake mkubwa tangu wakiwa shuleni.



    "Hongera sana kaka, ile kauli yako ya kwamba umefeli shule lakini hukufeli maisha naiona" aliongea John akimpa heko rafiki yake lakini Frank alijikuta ameganda ghafla sana mara baada ya kuona kitu kilichomfanya kushangaa, hali ile ikapelekea hadi John kuuliza kuna kitu gani kilichomfanya kijana huyo kushangaa.



    "unamuona yule binti mrembo anayeshuka kwenye ile gari ya gharama pale?" aliuliza Frank alipomuona binti mmoja mrembo sana akishuka kutokea kwenye gari ya thamani ya juu.



    "kwanini nisimjue Frank, yule ndiyo Jeny binti wa Rais Mobande, binti yule ni maarufu sana na amekuwa ni wa pekee sana, mara nyingi huwa anakuja hapa na amekuwa akinifanya mimi kupata habari za kuweka kwenye gazeti lililoniajiri" alisema John huku akitoa kamera yake ndogo ya kazi na kumsogelea binti huyo aliyekuwa anakuja maeneo hayo walipokuwa wamekaa wao. Alikuwa akichukua picha kadhaa kwa ajili ya kazi yake kwani John kwa kipindi hicho alikuwa tayari ni muandishi wa habari. Alipomaliza kidato cha nne hakuwa na alama nzuri za kumpeleka kule kuliko na malengo yake ya kielimu hivyo kuamua kusomea uwandishi wa habari ambayo nayo fani hii alikuwa akiihusudu sana wakati akiwa shuleni. Tabasamu la Jeny binti wa Rais ambaye alikuwa na wapambe wake wawili lilimfanya kumuona ni binti mrembo sana.



    Frank alikuwa ni kijana mzuri mwenye sura ya kuvutia sana, mabinti wengi walikuwa wakijigonga kwake lakini hakutaka kuwasikia hata kidogo kwenye maisha yake. Bado alikuwa na ndoto za kuhakikisha elimu yake inakuwa kubwa si hapo tu alipofikia. Kitendo kile cha Frank kumtazama yule binti, Jeny aliachia tabadamu pana lililotoka moyoni kabisa lakini Frank hakuwa mtu wa shobo hivyo ageuza sura yake kando ili kuepusha kuanzisha urafiki na watoto wa wakubwa kwani kila akikumbuka kichapo alichopewa siku ile alipokuwa akitokea shule, aliamini asilimia zote kuwa watu wenye pesa ni watu wenye dharau siku zote.



    "Amekaa benchi la hapa nyuma yetu, si kawaida kabisa ya binti huyu maarufu kukaa kwenye eneo hili mara nyingi yeye hukaa kule V.I.P. Sasa leo napata ajabu sana kumuona amekaa mahali hapa" aliongea John mara baada ya kuwa ametoka kuchukua picha za binti huyo maarufu ambaye alikuwa akija kwenye fukwe hiyo kubwa ambayo watu huingia hapo kwa kiingilio na huwa wakishuhudia burudani mbalimbali.



    "Achana nae John hebu tuzungumze yetu yaliyofanya tukutane mahali hapa na siyo kumzungumzia mtu huyo, ameshakuwa ni mtoto wa Rais wa nchi tayari inatosha lakini si kumfanya mtukufu hivyo" alisema Frank na alionekana kuwa hakuwa akipenda tabia ya kushobokea watu wenye pesa kabisa katika maisha yake. John alilijua hilo na alifahamu fika kuwa rafiki yake hakuwa rafiki na watu maarufu.



    "Frank my friend!" aliita John. Frank akamtazama rafiki yake huyo usoni, John akaendelea.



    "Samahani kwa kutokukupa taarifa ya kuhitaji kukutana nawe mahali hapa, unaona watu walivyojaa kiasi hiki?" akaacha swali John, Frank akatikisa kichwa chini juu kuashiria kuwa ameona, kijana huyo akaendelea tena.



    "Leo kuna uzinduzi maalumu hapa. Hii fukwe au hiki kisiwa kimenunuliwa na Kiongozi wa Serikali na ni waziri mkuu wa Taifa hili hivyo leo ni siku pekee sana. Tegemea kuwaona viongozi wakubwa wa kiserikali hata rais pia nimesikia atakuwepo hapa ikiwa ni kama kuja kumpa hongera waziri wake kwa kuweza kumiliki mali ya nyumbani na si kuwaweka wawekezaji. Pamoja na kuwa nitakuwa kazini kwani kuna picha nyingi nitakuwa nikipiga ikiwemo na kuwahoji viongozi hao lakini nilitaka na wewe uwepo hapa" alimaliza kuongea John, Frank akatabasamu tu bila kutia neno. Hakushangaa kwani hiyo hasa ndiyo ilikuwa tabia ya rafiki yake, kufanya mambo kwa kushtukiza, haikuwa mara yake ya kwanza.



    Muda si muda, magari ya askari jeshi pamoja na polisi yalianza kuingia hapo ufukweni kisha msafara wa magari machache ukifuatia. Magari hayo yalisogea hadi mahali palipoandaliwa kwa ajili ya kuegeshea magari kisha ulinzi ukawekwa mahali hapo na vingozi wakubwa wakaanza kushuka. Backa ambaye ndiye Waziri mkuu na mwenyeji wa eneo hilo kwa kipindi hicho, alikuwa tayari kumbe ameshafika hapo. Alitoka kwenye banda moja la makuti akenda kuwalaki viongozi wenzake. Walikaribishwa viongozi kisha wote wakaelekea kwenye banda kubwa la makuti.



    "Twende huku sasa Frank tukashuhudie pamoja jina jipya la kisiwa hiki na mmiliki mpya akikabidhiwa" alisema John.



    "nitaendaje wakati huko watu wanaingia na utambulisho maalumu?" aliuliza Frank.



    "Shika hii kamera ndogo hakikisha uwe unapiga picha kama zile ulizokuwa unapiga wakati tuko shule. Chukua na hiki kitambulisho kivae hapa na ukifunike hakuna ulinzi wa kuweza kukikagua kitambulisho chako hapa, mimi ni muandishi ninayetambulika hivyo hata hili vazi linatosha kuniruhusu kuingia. Twende sasa" alimpa maelezo rafiki yake John kisha wote kwa pamoja wakaelekea ndani ya banda lile lililokuwa limepambwa sana siku hiyo. Hafla ile fupi ilianza rasmi, walipanda viongozi mbalimbali miongoni mwa waliohudhuria hapo. Kila mmoja alisema lile alilopenda kusema lakini kubwa ni kwamba kila mmoja alionesha furaha yake kulingana na jambo lile. Muheshimiwa raisi akasema yake ya moyoni na yeye kisha ukafuatia muda wa Mh. Backa kutoa shukurani zake za dhati kwa viongozi wenzake walioweza kumpa ushirikiano na kuonesha furaha zao juu ya jambo lile alilolifanya. Akakipa jina jipya kabisa kisiwa kile.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "kuanzia leo hii kisiwa hiki kitakuwa kikiitwa Backa Island" alisema. Shangwe zikaibuka, watu wakafurahi huku viongozi wenzake wakiwa wanafurahi. Picha ziliendelea kupigwa kwa kila muda. John na rafiki yake nao hawakuwa nyuma katika kutekeleza kile walichokikusudia mahali hapo. Frank alipiga picha kwa weledi mkubwa sana na alijua kuchagua matukio yale ya muhimu. Wakati akiwa anapiga picha ya mwisho ya viongozi walipokuwa wakiagana kwa kukumbatiana baada ya shughuli ile iliyokuwa imeandaliwa na waziri Backa kufika ukingoni, Frank aliguswa begani na mtu asiyemjua kiasi cha kusitisha kupiga picha hiyo. Akalazimika kugeuka, mshtuko wa wastani ukamkumba mara baada ya kuiona sura ya Jeny binti wa Rais Julio akiwa amempa tabasamu la haja. Hali ile ikamfanya apate kigugumizi cha ghafla. Binti wa Rais? Anashida gani na mimi huyu? alijiuliza lakini wakati akiwa anajiuliza bila majibu, akakutana na kauli iliyomuweka na mshangao zaidi.



    "nahitaji kupata picha ya kumbukumbu na wewe kwenye simu yangu" alisema Jeny.



    "Mi....mimi au?" akauliza kiajabu ajabu huku akiwa hajiamini. Binti wa Rais? Maarufu? Halafu awe na shida na yeye? Ilikuwa ni lazima agugumie kwa kigugimizi.



    "Wewe ndiyo, nimejikuta nikivutiwa sana na wewe, tafadhali kubali" alizidi kuonesha uhitaji wake Jeny.



    "Sa...sa...sawa hakuna shida, nani mpigaji sasa?" aliuliza Frank huku akijitahidi kuipunguza hofu moyoni mwake. Baada ya kukubali tu binti huyo, alimshika bega Frank kisha akakaa ubavuni mwake huku akiachia tabasamu pana sana. Frank naye hakutaka kuiharibu picha hiyo, aliweka tabasamu picha hiyo ikapigwa.



    "Oooh! Jamani asante sana ni picha nzuri mno na nimeipenda, ni kama uzuri wako umehamia kwenye hii picha" aliongea kwa furaha sana Jeny mara baada ya kuiona picha hiyo kwenye simu yake. Furaha ilikuwa kubwa sana kwa Jeny lakini hali ilibadilika kwa Frank mara tu alipotazama kwenye jukwaa lililokuwa limekaliwa na viongozi. Frank alishuhudia kwa macho yake kumuona Mh. Rais akiwa amefura kwa hasira hali ile ilimuogopesha sana. Mbaya zaidi ni pale alipomuona mlinzi mkuu wa Rais huyo. Sura. umbo lake pamoja na muonekano wake kwa ujumla ulimkumbusha kitu. Kipigo cha siku aliyokuwa akitokea shule. Aliikumbuka ile sura ilikuwa ni yule mtu aliyemshushia kipondo nusura amuuwe. Aliwaona wakiwa wanateta jambo na Muheshimiwa.



    "Mungu wangu!" aling'aka kwa hofu kubwa kisha akajichanganya na watu akamfuata rafiki yake.



    "John tazama Rais alivyochukia baada ya mimi kupiga picha na binti yake. Naomba tuondoke mahali hapa si salama tena" alisema Frank. John alipotazama kule lilipo jukwaa kweli aliona. Hakupinga walijiingiza kwenye watu kadhaa na kutokea kwenye mlango kisha wakachukua Bajaji na kutoweka eneo lile.



    "Punguza hofu Frank Mh. Rais hawezi kukufanya kitu kuhusiana na binti yake kwanza wewe ni mgeni kabisa kwenye macho yake sasa ataanzaje kukutafuta?" John alijaribu kumtoa rafiki yake hofu mara tu walipofika nyumba kwake. Alimuona rafiki yake huyo jinsi alivyokosa furaha kabisa.



    "Ni kweli ulisemalo John kuwa Rais hawezi kunitafuta mimi lakini kinachonipa hofu na woga ni Bodigadi (Mlinzi wake wa karibu)

    (Mlinzi wake wa karibu). wake, John!"



    "Ananini!?" akauliza kwa mshangao john.



    "Ni yule aliyenishushia kipigo cha Mbwa mwizi kipindi kile nafukuzwa shule unakumbuka?" aliongea Frank.



    "Mungu wangu! Nakumbuka Frank, yule si anakujua vizuri yule?"

    "Kabisa" alijibu Frank.



    "Lakini usiwaze, ni muda mrefu sana umepita tangu kipindi kile hadi sasa, sidhani kama anaweza kukukumbuka. Kaa mbali na yule binti tena asikuzoee kabisa sawa?" aliongea John kumpa rafiki yake moyo na kumpunguzia hofu aliyo nayo. Ile ikawa siri yao pekee na wala Frank habari zile hakuzifikisha kwa wazazi wake. Hakujua kama kufanya vile ilikuwa ni balaa kubwa anajijengea ni bora basi angewaambia wazazi wake wangemwambia la kufanya. Alikaa kimya, kimya kilichomzalishia maumivu makali.



    *********



    "Kitema hakuna kitu ninachokichukia maishani mwangu kama kuchezewa binti yangu na masikini. Yule kijana mjinga ni nini anatafuta kwangu, akili zake za kuzaliwa anataka azilete kwenye familia yangu?" alibwata Julio alipokuwa Ikulu ametulia mbele yake akiwepo Kitema kijana mwenye mwili mwembambali lakini uliobeba roho nzito ya kuuwa.



    "Umesema unamjua vizuri yule Nguchiro?" akauliza Julio baada ya kumeza mate.



    "Ndiyo, ni yuleyule uliyemchezea mchezo hadi akashindwa kuendelea na masomo, pia ni yuleyule niliyekosa kumgonga na gari siku ile" alieleza Kitema.



    "Ndiyo maana nikakuambia siku ile ni bora ungemgongelea mbali kabisa, ona sasa alivyo kisebengo, huyu mtoto ni anaakili za kuumbiwa nazo na ninawasiwasi mkubwa sana kama ameanza ukaribu na binti yangu ni wazi atakuwa ni pingamizi kwangu baadaye, wewe unajua kuwa ninampango gani na Taifa hili hata kama miaka mia lakini ni lazima niliweke chini yangu" aliongea Mh. Julio kisha akatuama akanywa maji kwa pupa na kuitua gilasi ya maji ikiwa tupu mezani.



    "Kitema!" akaita, kisha kabla Kitema hajaitika akaendelea.



    "Hakikisha unajua huyu Kunguni mahali anapolala hadi anapotafutia ridhiki, ukishajua tutajua mtego wa kumtegea na safari hii tuna muuwa bila kuacha ushahidi, pumbavu!" alisema Mh. Julio. Kitema akasema hakuna shida kazi hiyo ni rahisi kwake na ataifanya kwa muda mfupi sana.



    Shughuli za usambazaji wa magazeti ikawa inaendelea bila shida yoyote. Frank alizidi kuifanya kazi yake bila ya kuwa na hofu. Alihakikisha majumba yote ya kifahari ya watu wasiopenda kutoka nje kwa kufuata huduma ndogo kama hizo za kufuata magazeti, wakiwa wanapata bila shida na kwa wakati. Siku kama ya nne hivi wakati Frank akiwa anasambaza magazeti pasipokujua kuna watu walikuwa wakimfuatilia, Aliingia kwenye jingo moja kubwa kama ilivyoada yake. Alifungua lango ambalo siku zote analikuta limeegeshwa tu kama hivyo kisha hujongea kwa mwendo mfupi tu hadi kwenye benchi moja lililopo mule ndani ya uzio. hapo huwa ndipo awekapo magazeti yanayohitajika kisha kuondoka zake lakini siku hii wakati anaacha hayo magazeti yanayotakiwa, Kitema alikuwa ndani ya Jumba hilo kwani humo ni mwanamke pekee aliyekuwa akiishi. Sasa kumbe mwanamke huyo alikuwa ni kimada wa Kijana huyo katili ambaye anauwezo hata wa kuamua kukuuwa tu kwa hila zake bila hata ya sababu za msingi kwa jinsi roho yake ilivyo na sifa ya kupenda kuuwa. Alichungulia dirishani kama bahati akamuona Frank akiacha magazeti kwenye benchi kisha kuondoka. Kitema akajua kumbe kazi yake ni ndogo kiasi hicho. Alizunguusha macho mule ndani akaona gazeti moja la udaku likiwa juu ya meza. Akalivuta na kulishika.



    "gazeti la nini tena huby, muda huu ndiyo unakuwa mtamu sana kufanya mapenzi, hadi ukifika muda wako wa kuondoka utakuwa umeshanitosheleza tayari" alilalamika mwanamke mmoja mrembo, mnene aliyekuwa amejiziba kifua chake kwa shuka nzito.



    "Najua wajubu wangu mrembo na wewe unanijua mimi vizuri.....haya magazeti huwa unayanunua muda gani maana shughuli zako wewe ni nyingi sana sidhani kama unamuda mzuri wa kuvifuata vibanda vya magazeti" aliongea Kitema kisha kuuliza mwishoni akiwa anataka kujipa uhakika kama kweli huyo kijana aliyemuona anakuja hapo kila siku.



    "kuna kijana ambaye huwa ananiletea haya magazeti na huwa nalipa kwa mwezi, anakuja hapa kila siku na anajali sana muda" alijibu huyo mwanamke bila kujua kama anamuuza mtu bila ya malipo. Kitema alipopata hilo jibu alijizugisha mahali hapo kwa kutania kuwa wanawake wanapenda sana habari za kidaku akalitupia gazeti mezani kisha kumkumbatia mwanamke huyo na kuanza kumpa raha hizo za asubuhi asubuhi.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Majira ya saa nne asubuhi ilimkuta Kitema kwa muheshimiwa Rais ambako ndiko kibarua chake kilipo. Pamoja na kazi ya ulinzi lakini pia alikuwa na kazi ya siri aliyokuwa akifanya na kiongozi huyo mkubwa wa nchi ya Ungamo.



    "Mkuu, yule kijana ni 'supplyer' na anasambaza magazeti karibia Mji wote huu, leo asubuhi nilipokuwa sehemu, nilimuona akileta magazeti" alisema Kitema.



    "Well done, sasa anakufaje huyo kijana na lini Kitema?" aliuliza Julio.



    "Atakufa kama kumsukuma mlevi tu na atakufa kesho" alijibu Kitema kisha kukamilisha mjadala huo.



    Siku iliyofuata asubuhi kama kawaida Frank alikuwa barabarani akielekea katika kusambaza magazeti baada ya kuletewa mzigo mkubwa wa magazeti mahali ilipo ofisi yake. Alisambaza kwenye nyumba nyingi kisha kuelekea kwa yule mwanamke ambaye huwa ndiyo mtu wa mwisho kumpelekea bidhaa hiyo. Wakati anaegesha pikipiki yake nje ya lango lile. aliona mlango ukiwa uko wazi hakuhoji sana kwani hali hiyo si mara moja wala mara mbili kukutana nayo. Aliingia ndani akiwa na haraka sana hadi mahali anapoacha bidhaa hiyo. Alipoweka na kugeuka ili kutaka kuondoka alishtuliwa na sauti nyuma yake ikimwambia kuwa asisahau kuweka na gazeti la michezo mahali hapo. Alipogeuka kumtazama mtu huyo, alikutana na sura ile asiyopenda kukutana nayo, sura aliyokuwa akiiogopa kama ukoma, sura yenye kumpa mawazo kila aifikiriapo. Kitema. Tena alikuwa akitabasamu huku akiwa anasogea taratibu akiwa amevaa bukta kubwa juu akiwa hajavaa kitu na kuuonesha mwili wake kama wa Fidodido, mkononi mwake akiwa amekamata bastola ndogo ya Ki-Japan.



    "Unataka kuwa mkwe wa Rais masikini wewe, au unataka kujenga ukaribu na familia ya rais ili iweje. Rais hakupendi wewe tokea zamani na amenituma roho yako leo hii" alizidi kuimba wimbo uliokuwa ukimpa Frank wazimu. Mwili wote aliuona kama siyo wake kwa jinsi ulivyokufa ganzi na viungo vya mwili wake kuanza kumtetemeka. Rais hakupendi wewe toka zamani na amenituma roho yako. akayafikiria yale maneno ya kijana yule Frank. Rais hanipendi tokea zamani? Nimemfanya nini mimi jamani? aliwaza namna hiyo lakini akashtuka.



    "Huna hata muda wa kusali sala yako ya mwisho nakuuwa now" sauti hiyo ndiyo iliyomshtua kijana huyo. Wakati kitema akisogea karibu ya Frank, kumbe yule mwanamke kule ndani alikuwa akisikia yale maneno hivyo akajua kuwa huwenda yule kijana akauwawa mbele ya macho yake tena nyumbani kwake. Akili yake iliamini kuwa ule ulikuwa ni wivu tu wa kawaida aliokuwa akiuonesha Kitema mahali pale. Akajua kuwa kama ataendelea kukaa ndani kweli kijana yule angeweza kuuwawa na yule mtu hivyo hakupenda itokee. Kitema alitoa usalama wa bastola ile kisha kumuelekezea Frank lakini wakati anamuelekezea kijana yule aliyejua kuwa hapo hawezi kuokoka na kifo hata kidogo, yule mwanamke alifika na kupiga kelele kumwambia Kitema kuwa kijana yule hakuwa na kosa lolote hivyo aache kumuuwa. Lilikuwa kosa. Kitema alishabadilika mahali hapo na hakuwa binadamu mwenye huruma tena. Zile kelele akazitafsiri kama usumbufu kichwani mwake. Aliigeuza ile silaha na kumchapa yule mwanamke risasi mbili za kifuani. Kitendo kile cha kitema kugeuza silaha na kupiga kifua cha yule mwanamke kilikuwa kimezimaliza risasi zilizomo ndani ya bastoka ile hata alivyoirudisha kwenye lengo haikukohoa kitu. Kitema alikasirika sana akaamua kuitupa na kumfuata Frank lakini hakuambulia kitu. Frank alikuwa ameshatoka zamani na alishaliwasha pikipiki lake kisha kuondoka mahali hapo kwa kasi kubwa. Kitema akabaki akiporomosha matusi mfululizo pasipo faida. Frank alikwenda hadi nyumbani kwa John akiwa na lengo la kumueleza kila kitu lakini kikubwa ni kuomba hifadhi ya muda hadi giza litakapoingia ndipo angetoka na kurudi nyumbani kwa wazazi wake kwa lengo la kwenda kuwaaga ili apotee kabisa ndani ya taifa hilo. John alisikitika sana alipopewa hizo taarifa hakujua Frank alikuwa na nini hadi kusakwa namna hiyo kama gaidi. Hakuwa na msaada tena wa kuweza kumsaidia kijana wa watu, alichokifanya ni kumuacha humo ndani kisha yeye kuelekea ofisini kwake.



    "Taarifa mbaya ya habari ikakumba masikio ya kila mwananchi kuwa eti, kijana Frank anatafutwa na polisi kwa kosa la kufanya mauwaji ya mwanamama mmoja tajiri kwa sababu za kijinga tu. Zilikuwa ni sababu ambazo hakuna hata raia ambaye hakuamini kuwa kijana huyo angeifanya. Taarifa zilisema kuwa, kijana huyo mwenye mwili wa kuwachanganya warembo, kinyume na biashara yake ya kusambaza magazeti lakini pia alikuwa na biashara nyingine ya magendo ambayo ndiyo iliyokuwa ikimpa kijana huyo mafanikio ya haraka. Kikubwa kilichowaacha watu vinywa wazi ni kwamba kijana huyo alikuwa akitoka kimapenzi na marehemu huyo na siku aliyokuwa akipeleka magazeti asubuhi, alimkuta mwanamke huyo akiwa anajivinjari na kidume mwingine. Hali ya wivu ikazaliwa kama upepo wa kiangazi. Kijana huyo ambaye alikuwa anamiliki bastola aliyokuwa akifanyia magendo yake ikiwemo unyang'anyi, alimpiga risasi dada huyo na kumsababishia kifo. Habari hiyo ilikuwa ni mwiba mkali sana kwa wazazi wa Frank ambao walikuwa wakimjua vilivyo kijana wao pia walikuwa wakijua hata kuishika silaha ya kwenye picha hajawahi, leo anaambiwa kaitumia kumuulia mtu. Lilikuwa ni jambo lisilokuwa la kweli na halingekuwa kweli labda kama watamlazimisha akubali tu. Si kwa wazazi pekee bali hata Frank mwenyewe alikuwa akishangaa na mwishowe kuamua kulia maana kwa tukio hilo ni wazi hakuna mtu ambaye angemuelewa kwa anaivyoijua jamii kwa kupokea vitu bila kuvifanyia uchunguzi, hakuna ambaye angemuelewa ni lazima wangezidi kumshutumu. Jioni John alirudi nyumbani kwake akiwa na mshangao na macho akiyatoa pima. Ile habari ilikuwa ni kichekesho sana lakini hakuwa na uwezo wa kucheka hata kidogo. Angechekaje wakati Frank muda wote huo alikuwa amebeba huzuni na hajui hatima ya maisha yake kila akifikiria.



    "Hii taarifa iliyosambaa mitaani ni ya kweli au? Mbona sielewi Frank?" aliuliza John.



    "Wewe unaionaje kwani?" alirudisha swali Frank. John akatulia kidogo kisha akasema.



    "Watakuwa wamekufananisha tu hawa watu"



    "Hapana hawajanifananisha bali wamekusudia kunipoteza kabisa kwenye hii dunia. Yale niliyokueleza asubuhi wameyageuza na kunibambikia mimi ili watimize lengo lao la kunitia mikononi mwao" alisema Frank. John akaelewa lakini hakujua jinsi ya kufanya. Alibaki kimya kabisa. Ilipofika saa mbili usiku, Frank aliamua kuaga hapo kwa rafiki yake akimwambia kuwa anaelekea nyumbani kwao ili akawaage aweze kutafuta pa kwenda kwani hayupo tayari kuingia mikononi mwa hao jamaa kirahisi ni lazima atoroke. John akamuuliza ni wapi atakapoelekea kwa usiku huo, Frank akajibu popote pale atakapokwenda ni sawa lakini siyo kupoteza maisha wakati bado anandoto za kuishi. John akakubali kishingo upande kwani hakuona njia ambayo angempa rafiki yake. Frank akapita njia azijuazo mwenyewe usiku huo hadi alipotokea nyumbani kwao. Ile anafika kwenye uwanja wa nyumba yao, akaoana gari ambayo haikuwa kawaida ya gari hiyo kuweka makazi hapo, hali hiyo ikampa pich ya kuwa kuna kitu bila shaka. Akanyata na kupitia upande wa nyuma wa nyumba yao akaja kutokea kwenye dirisha kubwa la

    la kuangalia ndani ya sebule. Aliogopa saona na moyo ulinza kukimbia kwa kasi kubwa.



    "Hakuna miujiza itakayokuja kwenu na kumifanya muokoke zaidi ya kuonesha kijana wenu alipo" Ilisikika sauti ambayo Frank aliifahamu bila shida, ilikuwa ni ya yule bwana aliyetaka kumuuwa asubuhi na muujiza wa Mungu ukamuokoa. Inamaana hawa jamaa wamedhamiria kuniuwa kweli? aliwaza kijana huyo pale dirishani huku akiwahimiza wazazi wake moyoni wasiseme.



    "Yuko wapi mtoto wenu eeh?" sauti ile ilisema kwa nguvu kisha kelele za maumivu kusikika pale baada ya Frank kushuhudia mama yake akipigwa ngumi nzito ya kifua hadi akapata shida kuitafuta pumzi.



    "Hatujui alipo jamani, tokea asubuhi alivyotoka hapa hakurejea tena, naomba mniachie mke wangu jamani mtamuuwa bure" aliongea baba Frank.



    "Kwahiyo unauchungu sana na mkeo si ndiyo?" aliuliza Kitema aliyekuwa amesimama katikati ya wazazi wa Frank waliokuwa wamekaa chini wakiyaacha makochi yao mawili yakiwa yamekaliwa na wanaume wawili waliojaa misuli.



    "Unampenda sana mkeo wewe, sasa tuambie ni wapi alipo kijana wako ili tusizidi kumtesa mkeo. Wapi kwani alikosema anaelekea?" akauliza tena Kitema lakini jibu likawa ni lilelile. Aisee! Kitema alichomoa kisu kwenye soksi za kiatu kwa kasi kubwa kisha akakizamisha kwenye bega la baba wa Frank. Uchungu mkubwa ulimkumba kijana huyo, machozi yalimtoka kwa wingi sana lakini hakuthubutu kilio cha sauti kimtoke. Alitoa simu yake ya kisasa kabisa na kuanza kuchukua matukio yote yalivyokuwa yakiendele. Kisu kile kilikuwa hakichagui pa kukita, kilikuwa kikitoka bega hili na kuhamia bega lile, kikitoka paja hili kinahamia paja lile. Baba wa Frank alilia hadi kilio kikamsaliti akabaki kuugulia maumivu moyoni na hatimaye wakamchoma kisu cha kifua kwakua aligoma kabisa kuongea. Adhabu ikahamia kwa mama yake. Hapo ndipo alishindwa kuvumilia Frank. Alishindwa kabisa kutazama kwani mama yuke alivuliwa gauni alilokuwa amelivaa kisha kila akiulizwa na yeye kusema hajui, basi chuchu moja ya titi lake ilikuwa ikikatwa bila ganzi na kuondolewa. Kitema alikuwa ni mnyama mbaya sana. Mama yule alikatwa chuchu zote kisha Kitema akasimama na kuwatazama wale vijana akasema.



    "Jamani hawa wajinga wanamapenzi mazito kwa mtoto wao hivyo wamegoma kabisa kumtaja alipo. Ni muda wenu sasa wa kumla uroda huyu mama kisha ndiyo tuna muuwa. Njooni mumuingilie na mumuingilie kweli hakuna kuchagua jinsi ya kumuingilia, faidini huyu kisha mimi nitakata kichwa chake na nitampelekea mkuu kumuonesha kuwa wamegoma kutuelekeza nasi tumemaliza hasira zetu kwao" alisema Kitema. Maneno hayo yakamfanya Frank alie vibaya sana kisha hakutaka kushuhudia huo unyama aliokuwa akitaka kufanyiwa mama yake mzazi mbele yake. Aliichukua simu yake kisha akaondoka kwa mwendo wa kulewalewa mithili ya mlevi wa Chibuku (ni aina ya pombe ya kienyeji). Matukio yale yalikuwa yamemlevya vibaya sana. Alitembea hadi alipofika umbali kidogo na nyumba yao akageuka na kuitazama kwa masikitiko makubwa sana akasema.



    "Baba na mama nendeni kwa amani ya bwana. Baba umekufa kifo kibaya sana mbele ya macho yangu na najua muda wowote kuanzia sasa mama nawe unakufa baada ya...yaa....aanghr!" alishindwa kumalizia Frank, uchungu wa kile anachokwenda kufanyiwa mama yake ulikuwa mkubwa mno, mama yake alipitia mateso makali kuliko baba yake lakini hakuwa na jinsi zaidi ya kusema kuwa.



    "Watalipa wote waliomifanyia unyama huo nikirudi ninakokwenda" kisha akageuka na kukimbilia mahali ambapo ni nje ya mji kabisa usiku huo. Frank wakati anakimbia hakutaka kuondoka bila kumpa taarifa rafiki yake kipenzi John kwani alijua fika akingoja hadi kukuche habari ingeweza kubadilishwa na ikawa kinyume chake kisha rafiki yake kumuelewa vibaya. Aliandika ujumbe kwenye simu kisha akautuma kwa John.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "NIMESHINDWA KUWASAIDIA WAZAZI WANGU KUKIEPUKA KIFO. WAZAZI WANGU WAMEKUFA KIFO KIBAYA SANA MBELE YA MACHO YANGU. RAIS AMENIULIA WAZAZI WANGU KISA NI MIMI TU, WAZAZI WANGU WAMEKUFA KWA MAKOSA YANGU. JOHN. BAKI NA SIRI HIYO MOYONI HADI PALE NITAKAPO KUJA KULIPA VIFO VYAO. UKIITOA KAULI HII KWA WATU KUWA RAIS NI MUUWAJI UJUE KUWA NITARUDI UKIWA UMESHAKUFA TAYARI. USISEME, NATAKA NIKIRUDI UNISAIDIE KAZI YANGU YA KULIPA KISASI. JOHN." ujumbe huo ulisema hivyo. Frank akawa wa porini maisha yake yote huku akiwa hajui ni lipi afanye kwa kipindi hicho kigumu. Baada ya muda wa kukaa huko porini huku akiwa anazipata habari kwa kusoma magazeti ambayo amekuwa akiyapata kwa kujibadilisha muonekano anapokuwa na shida ya kitu mjini, alipata taarifa ya kuwa Mtoto wa Rais anataka kufungua kampuni kubwa sana kwani alikuwa amesha maliza elimu yake ichini Marekani, inayohusiana na masuala ya mitindo hivyo alitaka kufungua kampuni kubwa inayohusiana na mambo hayo. Habari ile ikawa ni mkuki kwenye moyo wa Frank. Mimi sina furaha lakini Familia nzima ya Rais inafuraha kwa binti yao kuwa mwanamitindo mkubwa. Rais alinifanya mimi nisisome, alinifanya mimi nisiiletee familia yangu furaha pia akaamua kusababisha vifo vya wazazi wangu na kunifanya niishi kama Nyani msituni. Nakwenda kuizima hiyo furaha na nikishindwa kuizima furaha hiyo basi mimi nitajiuwa mwenyewe. Lazima binti wa Rais afe ndiyo nikimbie huu mji ikiwezekana Taifa kwa ujumla. Aliwaza Frank kisha akafikiri njia ya kuweza kumuangamiza mtoto huyo wa Rais anayekwenda kwa jina la Jeny.



    Siku ya juma pili, siku ambayo watu wengi hufika mahali penye bustani nzuri na kupata upepo. Ilikuwa ni bustani yenye hadhi ya juu sana na watu wengi maarufu walikuwa wakifika eneo hilo. Ilikuwa ikifahamika kama Happy Garden. Ilikuwa ni Bustani ambayo watu wa chini hawakuweza kufika maeneo hayo kwani gharama yake ilikuwa ni kubwa sana. Binti wa Rais pia alikuwa akipenda kufika hapo siku kama hii na tayari Frank alishafanya uchunguzi wake hivyo alijua siku hiyo ni lazima ngefika hapo kwa ajili ya kubadilishana mawazo na watu maarufu kama yeye. Frank alikuwa amesimama mahali amabapo ndipo gari zinapopakiwa na ilikuwa ni lazima uvuke reli ambayo ilikuwa bado ikitumika ndipo uelekee upande ulio na bustani hiyo. Frank alikuwa akilipigia mahesabu bonde ambalo lipo kama hatua kumi na tano kutokea hapo na mkononi alikuwa amekamata upanga mzito na wenye makali ya kutosha, huo ndiyo aliokusudia kufanyia mauwaji ya binti huyo wa Rais ambaye kwa muda huo ndiyo alikuwa anaingia mahali yalipo maegesho ya magari na gari yake ya thamani ya juu sana. Alikuwa akipiga mahesabu makubwa sana kijana huyo, kwa tukio atakalolifanya na jinsi atavyopotea hapo. Kama nikifika korongoni tu basi wamenikosa na hawataweza kunikamata abadani. Aliwaza. Alimuona Jeny akiwa anakuja akiwa na mpambe wake mmoja ambaye alikuwa nyuma yake siku zote. Alipokaribia ile reli tu akaonekana kujipapasa mifukoni mwake kuonesha kuwa kuna kitu alikuwa akikitafuta, ni kweli. Alikuwa amesahau kitu na muda huo huo akamuagizia mpambe wake akamletee kwenye gari na muda huo huo kukawa na Treni linakuja kwa kasi kubwa.



    "Hapahapa" akasema kwa sauti ndogo Frank huku akianza kutembea taratibu kumfuata Jeny. Alikuwa amevaa kama kichaa, nguo chafu vibaya sana na zilizochanika. Kichwani alikuwa amevaa kofia mbaya sana ya pama iliyochakaa. Treni lilipokuwa likikaribia, Frank akabadili mwendo sasa akawa anakimbia taratibu hatimaye akaongeza kasi. Treni lilipofika karibia na usawa wa yule binti, Frank alikuwa ameshafika pale na hakukuwa na aliyemtilia shaka. Kikumbo kikubwa na cha nguvu sana kilimkumba Jeny. Hammadi! Akajikuta hewani akielekea kwenye barabara ile ya Treni.

    "mamaaaa nakufaaaaaaa.....!" kelele hizo zilikuja kuzimwa na kishindo kikubwa cha kugongwa na Treni hiyo. Wakati watu wakiwa wanashangaa wasielewe na wakati huo yule mpambe ndiyo alikuwa akitoa kichwa kwenye gari akiwa ameshika simu mkononi ambayo ilionekana ndiyo aliyokuwa ameagiziwa garini, huku Frank alikuwa anajirusha korongoni na kuelekea kwenye mto mdogo. Alijitosa majini na kuibukia upande wa pili wa mto ule mdogo kisha kupotelea kwenye kichaka kidogo cha eneo hilo ambamo tayari alishajua akiingia hapo ni njia gani atapitia.



    Tabasamu kubwa liliuwamba uso wake huku akiwa ameshafuta machozi ya kutosha ambayo yaliacha ramani ya weusi kutokana na ngozi yake kuwa chafu sana. Alilia vya kutosha sana hasa alipoikumbuka simulizi hiyo ambayo ilikuwa ikimuumiza sana. Bado alingali palepale juu ya lile jiwe kubwa kijana yule mwenye muonekano wa mtu aliyechanganyikiwa akili. M.Y.S au kwa jina alilobarikiwa na wazazi wake alikuwa akitambulika kama Frank, kijana ambaye aliondoka Pande akiwa kwenye muonekano wa kichaa kisha kurudi tena akiwa kwenye muonekano uleule wa kichaa.



    "Julio Mobande Julio (J.M.J)" alitamka jina hilo Frank kichaa kisha tabasamu likafuatia, aliporidhika na tabasamu lile, akaongea tena.



    "Nimerudi kwa ajili yako sasa na nchi yangu kwa ujumla, najua ulikuwa ukihitaji nife kwa gharama yoyote ile lakini umefeli, utakufa wewe na muda wowote ule lazima kifo cha wazazi wangu kilipwe" aliweka tuo kisha akalitazama korongo lile refu ambalo ndilo kimbilio lake hasa huko mjini kunapowaka moto. Frank kichaa alitia mkono mfukoni mwake akatoka na kipande kidogo cha picha ambacho alikitazama kwa muda akatikisa kichwa kisha akachomoa peni kwenye mfuko mkuukuu wa shati akaupiga alama ya 'X' ile picha. Akanong'ona moyoni.



    "Naanza na wewe kunguru mweusi kisha namgeukia yule mwenzako kabla ya kurudi kwa yule kimbaumbau Kitema. Picha hiyo ilikuwa ni ya mmoja kati ya wale mabwana wenye misuli minene ambao ndiyo waliomuingilia mama yake kwa sifa kabla hajakatwa kichwa chake. Frank kichaa aliruka kutoka pale kwenye jiwe akaporomokea chini kisha akadanda kwenye Gema moja kubwa akakamata barabara ya chini ambayo ilikuwa ikipita watu mbalimbali kwa ajili ya matembezi ya kwenye makorongo yale na maporomoko ya kipekee ya mto. Alikujakutokea juu upande wa kushoto tofauti na pale alipojirusha siku aliyokuwa akiagana na Petii. Breki ya kwanza ilikuwa ni kwenye nyumba moja kubwa ambayo ndiyo waliokuwa wakiishi wale mabwana wawili wenye misuli. Haikujulikana ni wapi aliyapata maelekezo hayo. Majira hayo alijua kabisa hawezi kuwakosa watu hao, kweli hakukosea. Alisikia sauti nene ndani kisha sauti hizo, hujibiwa na sauti nyembamba. Akachungulia kupitia dirisha akawaona mabwana wale ambao ndiwo alikuwa akiwahitaji hasa wakiwa wamejiachia kwenye makochi yaliyopo sebuleni hapo. Akanyonga kitasa kisha akavamia kwa kishindo kikubwa akiwa na bastola ya pekee mkononi mwake. Wale mabwana hawakuwa wametegemea uvamizi ule hata kidogo, hivyo wakati anavamia, ni sauti za kuomba msaada kutoka kwa wale mabinti ndizo zilizosikika mahali hapo. Bwana mmoja akaleta ukidume. Akatoka kwenye kochi alilokalia ambalo alikuwa akimchezea binti mmoja kwa atakavyo, akajifanya kutaka kurukia silaha iliyopo mezani. Kosa kubwa la jinai alilifanya. Risasi kavu ikachangua mabega yake mawili, yule bwana akajimwaga chini huku akitokwa na ukelele wa maumivu.



    "Najua hamkumbuki chochote nyie wajinga, najua hilo lakini kumbukeni kuwa, mla ndizi hakumbuki siku ailayo Ndizi lakini yule mtupa maganda hukumbuka maana kila apitapo huliona. Mlifnya kila mtakalo kwa wazazi wangu, mkanfanyia ushetani mama yangu wajinga nyinyi" alisema Frank kisha akamwaga njugu kama mchele kwenye hilo eneo, aliwachakaza vibaya sana kwa risasi wale wajinga na kupotea anapopajua yeye mwenyewe huku akiwaacha wale wanawake wawili wakiwa hawaamini macho yao.



    ********



    Roi baada ya kutoka kwenye mihangaiko yake, alimkuta Petii akiwa yuko fiti kiasi. Zile dawa alizompa zilikuwa ni za aina yake sana, zilikuwa zinauwezo mkubwa wa kuondoa maumivu kwa haraka na kukufanya ujihisi ukosafi kabisa. Roi alifarijika sana kwa hali ile aliyomkuta nayo binti huyo.



    " Nadhani uko sawa kiasi?" aliuliza Roi.



    "Hapana siyo kiasi, nipo sawa kabisa hapa kinachotakiwa ni kuongeza mazoezi kwa kiasi kikubwa ili kesho niingie tena kazini muda umekuwa si rafiki tena kwangu" alijibu, jibu ambalo lilifanya Roi kuanza kumpa maswali ya udadisi binti huyo. Petii hakuona haja ya kumficha kijana huyo kwani hadi hapo alijua fika kuwa huyo ndiye mtu wa pekee wa kuweza kujua tofauti na mwingine yoyote yule.Akaeleza sababu za kuja hapo Ungamo.





    Hakuna kitu kingine ambacho kilimfikisha hapo zaidi ya kazi ya kipelelezi kisha kuhakikisha anamtia mikononi Waziri wa ulinzi wa Taifa hilo ikiwezekana kumuuwa kabisa. Alieleza kuwa, waziri huyo anayefahamika kwa jina la Bande Sir, Alikuwa ni mtu mwenye sifa mbaya sana alipokuwa nchini Malawi. Alikuwa akifanya kazi ya kukodiwa kwa ajili ya kufanya mauwaji tu na kule alitumwa kwenda kumuua mtoto wa Waziri mkuu wa nchi ile ya Malawi na kazi hiyo alitumwa na mfanyabiashara mmoja mkubwa sana kutokea nchini huko ambaye hakujulikana ni nani. Kweli alitekeleza hiyo kazi akiwa na wenzake wawili na inasemekana wote wamekimbilia ndani ya nchi hii ya Ungamo mara baada ya kutoka chini ya mikono ya Polisi.



    "Muliwakamata kisha wakatoroka chini ya mikono ya Polisi?" aliuliza Roi.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Ndiyo, baada ya kufanya tukio la mauwaji chuoni, taarifa zikasambaa kwa haraka sana hivyo nikapewa hiyo kazi ya kuhakikisha hawavuki mipaka ya Malawi bila kuingia mikononi mwangu. Tukamwaga askari kila kona na taarifa zikaja kuwa wote watatu wameonekana uwanja wa ndege. Nilipofika pale nilikuta wawili mmoja alitoweka kimaajabu sana ambaye hata hapa sijafanikiwa kujua wapi naweza kumpata na hata sijui ni yapi makazi yake" aliongea kwa urefu sana Petii. Walijadili kila njia kisha wakapanga mikakati lakini yote hayo wakati yanafanyika Roi hakujitambulisha kwa petii kuwa yeye ni nani. Alijmbulisha kwa utambulisho wa kughushi japo jina lake aliliweka hadharani lakini hakutaka mtu yoyote ajue kuwa yupo hapo kwa kazi gani.



    "Nimependa kukupa msaada na nitaendelea kuwa na wewe bega kwa bega hadi mafanikio yako uyaone na uyafurahie lakini ningependa uniambie kuwa hadi sasa umefanikiwa kwa hatua gani?" aliongea Roi kisha kuuliza.



    "Kiukweli hadi sasa nimefanikiwa kwa aslimia ndogo sana kwani hadi muda huu niliyemgundua ni Bande Sir pekee hao wawili bado" alijibu Petii. Kimya kikatanda, hakuna aliyeongea hata mmoja mahali hapo walibaki kutazamana tu huku kila mmoja akimjengea mwenzake picha kwa namna yake. Muda ulikuwa umekwenda sana, giza lilikuwa tayari limeiteka anga. Ilipata saa mbili za usiku. Roi alijinyanyua akamtazama Petii usoni kisha akamwambia anatoka lakini angerudi muda wowote. Petii hakujibu kitu wala kuuliza alibaki tu kumtazama kijana huyo kwa macho ya kumtamani. Roi akatoka humo ndani kwa mwendo wa kawaida hadi kwenye maegesho ya magari, akaingia kwenye gari yake aliyokuwa ameiegesha mahali hapo kisha akatoweka. Kichwani mwake alikuwa amepanga kwenda kwenye Jumba kubwa alilokuwa akiishi Backa kabla ya kutekwa. Alihitaji kupata mambo kadhaa ambayo yangeweza kumpa mwanga wa ziadi. Alifika ufukweni akaegesha gari yake mahali kisha akajongea hadi kwenye Boti moja ndogo iliyokuwa ikitumika kutembeza watu majini.



    "habari yako kijana?" alisalimia Roi.



    "habari nzuri kaka karibu?" alijibu salamu kijana huyo aliyeonekana ndiye naohodha wa boti hiyo.



    "Ok, asante, nahitaji huduma lakini kabla sijaingia kwenye usafiri wako ningependa kujua kama utaweza kunifikisha kwenye kile kisiwa pale" alisema Roi, yule kijana akamuangalia Roi kwa macho ya kumsoma kisha akamuuliza kama alikuwa mgeni maeneo yale. Macho yake yalikuwa na zaidi ya hilo swali ilionekena dhahiri kulikuwa na kitu alikuwa akikificha ndani ya kifua chake lakini kwa mtu makini kama Roi haikumpa tabu kujua. Kijana yule alionekana kushangaa sana mara baada ya Roi kutaka huduma ile si kama alishangaa kwa sababu ulikuwa ni usiku, laa! Kilichomshangaza ni kijana yule kuhitaji kuelekea kwenye kisiwa cha Backa usiku ule. Taa zilikuwa zikiwaka kila upande wa lile eneo na huduma ya kuwatembeza watu ilikuwa ikiendelea kama ada, usiku haukujaliwa hata kidogo na kulionekana kuchangamka sana kiasi cha kwamba ungeweza kusema kuwa haukuwa usiku.



    "yaa, mimi ni mgeni eneo hili sijawahi kufika hata kidogo maeneo haya japo nimesikia kuwa ni maeneo mazuri sana kwa ajili ya kukimbiza mawazo kama yamekuzonga" alijibu Roi huku akiwa anamtazama kwa makini sana kijana yule.



    "Unaonekana kweli ni mgeni na hujui kuwa pale pamewekwa ulinzi mkali sana kiasi kwamba hakuna hata mtu mmoja anayethubutu kutia pua pale" alijibu yule kijana huku akiendelea na shughuli zake.



    "hakuna namna yoyote ya kuweza kunifikisha pale brother, naweza kukulipa kiasi utakacho, shida unifikishe tu kwenye kile kisiwa halafu wewe utarudi" kauli hiyo ya Roi ilimfanya yule jamaa kuacha shughuli aliyokuwa akiifanya kwa muda na kusimama kisha akamtazama Roi kwa umakini zaidi. Akataka kusema jambo lakini akachelewa.



    "nitakupa shilingi elfu arobaini kwa kunipeleka tu"



    "Elfu arobaini!" akashtuka.



    "ndiyo" alijibu Roi huku akiingia kwenye ule usafiri kwani alijua kwa kiasi hicho huyo kijana asingekubali kukiacha.



    "Kiukweli ulinzi wa pale ni mkali sana lakini kwakuwa hii ni kazi na niliianza tangu na tangu, kuna sehemu nitakupitisha na hakuna mtu ambaye atatuona....wewe ni askari?" aliongea huyo kijana kisha akachomekea na swali la mtego. Roi akajibu kuwa yeye hakuwa askari ni raia wa kawaida tu, akaongezea pia kuwa alikuwa anatamani sana kufika maeneo yale siku moja hivyo ameona si vibaya akatimiza adhma yake hata kama pana ulinzi kiasi gani. Yule kijana akacheka sana kisha akaongeza mwendo wa kile chombo. Mwendo ukawa makali kiasi. Walikuwa wanacheza mchezo wa kukizunguuka kile kisiwa kwa mtindo ambao hata kama walinzi waliowekwa wangekuwa wanakifuatilia wasingeweza kugundua kuwa hao walikuwa wakielekea eneo hilo. Baada ya kama dakika kumi, chombo kile kikapiga Nanga upande wa nyuma kabisa wa kile kisiwa, huko kulikuwa na giza sana hivyo ilikuwa ni ngumu sana kukaa walinzi kutokana na mazingira yake yalivyo. Roi akashuka sambamba na yule kijana ambaye alikuwa akimpa maelekezo kuhusiana na kisiwa kile jinsi kilivyo kisha wakaagana yule bwana alikuwa akiondoka mahala pale. Wakati akiwa anaondoka Roi alikuwa ameshapotelea kwenye giza zito, kutokana na nguo nyeusi alizovaa ikawa ngumu sana kuweza kumuona hivyo yule nahodha, alipoona abiria wake hamuoni akajua ameshapotelea ndani tayari kumbe si hivyo. Alitoa simu ya kiganjani yule kijana kisha akawa anabofya namba fulani wakati akiwa ameshabofya kitufe cha kusikilizia na kuiweka sikioni, akaguswa na chuma cha baridi mgongoni.



    "naomba hiyo simu tafadhali na usiongee kitu chochote, ukithubutu kuongea nahamisha ubongo wako kwa risasi" sauti nzito ya Roi ilizungumza nyuma ya yule kijana lakini kijana yule akacheza mchezo wa kupoteza ushahidi. Aliidondosha ile simu kutokea sikioni hadi chini kisha akaikanyaga na kuivunja kabisa. Roi akajua watu hao anaowatafuta walikuwa wajuzi wa kazi na walikuwa wako radhi kufa wao wenyewe kuliko kuonesha njia ya kumfikia mwingine. Wakati akiwa anawaza hilo yule kijana akajizungusha kwa teke kali lakini Roi alilitambua hilo, akarudi nyuma kwa kasi ya aina yake kisha akaruka mbele kwa haraka hiyohiyo na kutoa zawadi ya ngumi kavu ya mdomo, jamaa akagumia mmmh! kisha akatema damu na meno kadhaa. Akiwa anataka kuleta mashambulizi alitulizwa kwa ngumi mbili za tumbo zilizomfanya ainame kwa maumivu. Roi akamuwekea bastola kichwani.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Wewe ni nani?, mlinzi, askari, au nani niambie haraka sana maana muda uliopo ni mdogo sana?" aliuliza Roi. Badala ya kujibu yule kijana, vilevile alivyoinama, alijizunguusha na kumpiga teke moja la mbavu Roi ambalo alilisikia vizuri sana kisha kijana yule akajikunjua na kurusha ngumi kama tatu hivi ambazo mbili pekee ndizo Roi alijitahidi kuzikwepa lakini moja iliingia kwenye kifua kiasi cha kumyumbisha. Yule kijana ni kama alikuwa amepandisha mori, hakuja kwa kutulia kila sekunde aliitumia kupeleka mapigo. Roi alipoona mchezo umemgeukia akarudi nyuma kwa kasi sana lakini huyo kijana naye hakutaka kubaki, alikuwa anakuja hivyohivyo kwa kasi.



    "Bwege utanisumbua sana wewe" aliongea Roi akiwa ameigamia bomba moja la chuma.



    "umeingia pabaya sana mjinga wewe, unadhani utapata kitu hapa, hapa utakufa kabla hujaokota chochote" alibwata huyo kijana kisha aka-jump hewani kwa mtindo wa kupendeza akiwa na lengo la kumpiga Roi pigo moja maridhawa la ki-brazil. Roi akainama kwa wepesi wa hali ya juu na kuhama kabisa lile eneo yule jamaa akajaa kwenye lile bomba, akatokwa na mguno mkubwa wa maumivu, Roi hakumkawiza alimpiga ngumi nzito sana ya kwenye uti wa mgongo yule boya akalegea.



    "Mjinga wewe, unadhani ninamuda wa kupoteza hapa" aliongea Roi huku akiokota bastola yake na kuifutika kiunoni. Akakimbilia kwa upande wa mbele, alipochungulia kwenye kona moja hivi, akaona hakuingiliki hata kidogo, polisi walio katika sare walikuwa wakila doria kwa kupishana. Akarudi upande wa nyuma huko nako kukawa hivyohivyo. Akatulia kidogo. Alipotulia kwa muda, akatazama ule ukuta akaona kumbe kulikuwa na madirisha ya vioo akafanya cha kueleweka. Alifungua Rasket yake nyeusi aliyokuwa ameivaa mgongoni akatoa Gloves maluumu akazivaa mikononi, gloves hizo zilikuwa na uwezo wa kushika ukutani kutokana na jinsi zilivyotengenezwa. Akadandia ukuta na kuanza kupanda kwa kasi ya namna yake hadi alipolifikia dirisha moja, akavuta kioo kimoja na kujipindua kisha akazama ndani kwa kishindo kidogo kabisa. Jumba lote lilikuwa likiwaka taa masaa ishirini na nne kuanzia nje hadi ndani. Akapita chumba hadi chumba kijana huyo. Hakuna chumba ambacho alikikuta kipo katika usalama kila chumba kilikuwa kimetawanywa vya kutosha kuonesha kuwa vilikaguliwa na watu waliokuwa wakitafuta kitu fulani ndani ya jumba hilo. Roi alipopita kila chumba akatokea sebuleni huku bastola yake ikiwa mkononi lakini wakati anafika sebuleni hapo, kuna kivuli cha mtu alikiona kikiwa kinapotelea kwenye chumba kimoja hivi kilicho wazi, chumba hicho kilikuwa chumba cha jiko. Roi akaikamata vizuri silaha yake akanyata hadi kwenye mlango wa chumba kile akatulia tuli akisubiri mtu aliyeingia ndani humo atoke. Alitulia hapo kwa muda wa dakika moja nzima lakini hakukutoka mtu wala chakalachakala za kuwepo kwa mtu humo ndani hakuzisikia.



    "Kanitega au?" alijiuliza Roi lakini hakungoja. Alijisogeza kimya kimya akitanguliza kiatu kimoja badala ya kingine hadi alipoingia ndani humo. Akakagua kila upande wa chumba hicho kimya, nyuma ya mlango, kabati la vyombo, kimya. Macho yake yakatua kwenye dirisha la hapo jikoni, lilikuwa wazi.



    "Kapitia hapa huyu bwege, ni nani sasa....lakini hakuniona?" akajiuliza kisha akachungulia pale dirishani akaona Boti ndogo mfano wa pikipiki ikipotelea majini. Akachungulia kila kona ya upande ule, kulikuwa kimya sana.



    "Hakuna ulinzi hapa, ulinzi gani huu kama kila mtu anaingia na kuondoka awezavyo. Na huyu ndiye aliyechangua humu ndani, alikuwa anatafuta nini?" akajiuliza tena lakini alipokumbuka kuwa hata mtu mwenyewe hakumjua, akajua hawezi kujua alichokuwa akitafuta. Akaliacha hilo jiko hivyohivyo kisha akarudi tena sebuleni. Damu zilizogandamana zilikuwa zimejaa kwenye sakafu ya eneo hilo, akajua bila shaka kabla ya kutekwa kwa Backa palikufa mtu au palipigika mtu vibaya sana. Akazungusha macho yake kila kona ya eneo hilo kijana huyo machachari kisha akajikalisha kwenye kiti cha thamani ambacho kwa mara ya mwisho kilikaliwa na Backa mwenyewe siku ambayo alikuwa anatekwa.



    "Nini kilitokea? Inavyoonekana kuna mtu alikaa hapa na kukamatiwa hapahapa" alijisemea mwenyewe kwa sauti ya mkono wa birika kisha akayazunguusha macho yake kwa utaratibu sana na kwa kila pembe ya ile sebule. Nyumba hiyo ilikuwa haijatolewa kitu hata kimoja hadi rimoti zilikuwemo na bila shaka hata huo ulinzi ni kwa ajili ya kulinda mali za waziri huyo wa zamani. Nyuma ya meza iliyokuwa ikikaa meza ya luninga na redio kubwa, kuna kitu kama kijidirisha au kijitundu fulani ambacho hakikutoke kwa upande wa pili, ilikuwa ni ngumu sana kuona lakini macho ya Roi yaliona kitu.



    "Ile ni nini pale na mbona imefichwa pale? Ile ni simu tena ya kisasa zaidi kwanini iwe pale?" alijiuliza kijana huyo huku akiamka na kuifuata simu hiyo.





    "Yaa, ni simu kweli tena ni mpya kabisa" alijisemea baada ya kujua kuwa ilikuwa ni simu kama alivyodhani yeye. Ilikuwa ni simu ya aina yake, mpya na ya kipekee mno. Simu hiyo ilikuwa na uwezo wa kurekodi kama mtu uliyempigia ulitaka kumrekodi lakini upekee wa simu hiyo ni huu hapa, simu hiyo ilikuwa inauwezo wa kuihifadhi 'recording' hata kama hujaihifadhi wewe mwenyewe na inafanya kazi hiyo baada ya muda wa masaa mawili pasipo muhusika kuihifadhi rekodi hiyo. Roi alijaribu kuiwasha simu hiyo ikawaka alipotazama chaji, ilikuwa bado inachaji ya kutosha, hii inamaanisha kuwa simu hiyo ilijizima yenyewe baada ya kutokutumika kwa muda fulani. Akaikagua ile simu kwa muda kisha akaizima tena, akaangaza tena macho yake hapa na pale hakuona kitu kilichomfaa, akachomoka humo ndani kwa kupitia njia ileile aliyojia. Akafika kwenye ule usafiri uliomfikisha pale, akajipakia na kukamata usukani mwenyewe akarudi ufukweni ambako kwa muda huo kulikuwa kimya sana. Alipofika mahali ilipo gari yake, akaikagua kwa muda kidogo akiwa kwa umbali fulani alipohakikisha usalama, akalisogelea akafungua mlango na kutoweka. Alifika hotelini ukiwa ni usiku mkubwa sana lakini kulikuwa kunauwezekano wa kufika kwenye chumba chake kwa njia azijuazo yeye. Alifanya hivyo na kwa muda mfupi tu alikuwa ndani ya chumba chake. petii akashtuka kutokea usingizini akiwa na silaha mkononi lakini Roi hakushtuka ndiyo kwanza alikuwa akipunguza nguo zake na kuelekea bafuni kuoga. Alitumia muda mfupi sana kuweza kuoga akarudi chumbani.



    "Saa nane muda huu, ulikuwa wapi?" aliuliza Petii.



    "Nilikuwa kwenye starehe si unajua mimi si mwenyeji sana wa mji huu sasa ni lazima unizoee" alijibu Roi.



    "Kwaiyo hapo nafsi yako nyeupe na umemaliza starehe zote?" aliuliza tena Petii.



    "Hapana sio zote bado moja tu ambayo ni utamu wako si utanipa au bado unajisikia vibaya?" alihoji Roi huku akiwa anamsogelea mrembo huyo mwenye uzuri na umbo la kuvutia kisha akapanda kitandani na kumuweka chini yeye akiwa juu.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Nilijua tu ukirudi lazima unisumbue, hebu toka huko" aliongea Petii huku akijitahidi kumtoa Roi pale juu.



    "Kwahiyo umeshajua kuwa mimi ni msumbufu kwa muda mfupi tu tuliokaa wote hapa na hauko radhi kunipa utamu wako, acha roho hiyo wewe cha binadamu kimeumbiwa binadamu" alichombeza Roi huku akimpa mdomo huyo binti. Petii alijikuta akiupokea mdomo huo mwenyewe na kuanza kupeana ladha ya sharubati ya asili. Kila mmoja alionekana kuwa na uchu sana na mwenziye. Utamu ulikuwa ukikolea kila baada ya muda, hamu ya kuzidi kuufanya mchezo huo usiyo na bingwa ikawa inazidi kwa kila mmoja.



    "Unajoto tamu sana Petii" aliongea Roi kwa sauti ya mahaba.



    "Usinipake mafuta kwa mgongo wa chupa baby?"



    "kweli vile sikutanii" alizidi kuonesha kuwa anachokiongea hatanii. Wakazidi kujikunja hatimae miguno ikaongezeka. Asubuhi kulipokucha Roi alikuwa wa kwanza kukurupuka akakimbilia bafuni aliporudi, akamkuta huyo binti akiwa macho tayari.



    "Wapi hiyo mwanaume?" aliuliza Petii.



    "Bado kuna kazi sijaiweka sawa jana hivyo ni lazima nihakikishe naimaliza, vipi wewe?" alijibu Roi kisha akaacha swali.



    "kuhusu mimi usijali, tutakutana hapa jioni" alijibu Petii huku na yeye akijinyanyua akaelekea bafuni pia. Roi akatoka lakini pia Baada ya muda mfupi Petii naye akatoka. Dakika kumi na tano mbele, zilimkuta Roi mbele ya jumba la marehemu Ndungai. Lilikuwa halikaliwi na mtu tena na lilionekana halikuwa na ulinzi wa aina yoyote. Gari moja Toyota Hilux ambayo ilikuwa haina upepo ilikuwa imekaa kimya huku pembeni yake kukionekana gari nyingine ambayo ilikuwa imefunikwa na Turubai jeusi. Mlango ulikuwa umerudishiwa kidogo tu. Hapo Roi machale yakamcheza. Alihisi hali ya hatari kichwani mwake. Kuna mtu ndani. Aliwaza kisha akabadili njia ya kupita, alizunguka hadi upande wa nyuma, huko kulikuwa na chumba kidogo mfano wa stoo. Akagusa dirisha akalisukuma, dirisha hilo likasukumika, uwazi huo ukawa unamtosha kabisa kupita. Akatazama kulia na kushoto hakukuwa na mtu, akakamata juu akajivuta akatanguliza miguu na kuzama ndani kimya akatulia. Mlango wa chumba hicho ulikuwa umefungwa kwa komeo la kisasa kabisa, hakuwa na shida sana na pale stoo, shida yake kubwa iliyomfikisha hapo ni kutaka kujua kama kuna jingine la ziada ambalo angeweza kulipata. Akatekenya mlango lakini kwa tahadhari kubwa kisha akanyonga kitasa na kuusukuma ule mlango akapita taratibu kisha akaurudisha. Alikutana na korido moja ndefu akaifuata hiyo korido hadi mwisho akakunja kulia akakutana na sebule kubwa sana lililoonekana kuchanguliwa sana. Akaisogelea meza moja iliyoko pembeni ambayo haikuwa tupu. Ilikuwa na makaratasi ya kila namna, akataka kukaa ili ayapitie makaratasi hayo, akasikia sauti ya mlango uliokuwa unafunguliwa. Haraka sana silaha mkononi kisha akaruka kwa hatua ndefu, akakunja kwenye mlango mmoja uliokuwa wazi akatokea kwenye kijisebule kidogo ambacho kilikuwa kinakutoa nje. Akaona ule mlango ukiwa unajifunga na kujifungua wenyewe. Mh? akagumia.



    "kuna mtu katoka muda huu, ni nani?" akajiuliza mwenyewe kisha akaongeza kasi huku silaha yake ikiwa imara mkononi, alipoukaribia ule mlango kabla hajaufungua, akasikia gari ikitiwa moto. Akafungua haraka mlango, akaona ile gari iliyokuwa imefunikwa na Turubai jeusi ikiondoka. Haraka sana akalipiga picha lile gari kwa nyuma, akaiacha iende.



    "Ni nani huyu ambaye kila ninapofika anakuwa ameniwahi?" akajiuliza Roi lakini jibu hakulipata. Lakini wakati hayo yanafanyika kimya kimya, Petii hakuwa mbali na tayari alishaanza kuhisi kitu kwa Roi, aliamini kitu kimoja. Kama Roi si mpelelezi basi kuna jambo ambalo alikuwa akilifuatilia. Hivyo wakati yeye akiwa anapiga picha lile gari na kuliacha liende, Petii alikuwa ametulia kwenye gari yake ndogo nyuma kidogo ya duka la Pembejeo. Ile gari ilipopita pale akaifungia tela hadi ilipokuwa inaelekea. Gari ile ilikwenda moja kwa moja hadi mjini kisha ikaegeshwa kwenye jingo moja kubwa lililokuwa na uzio mkubwa wa michongoma. Petii hakutaka kujua mengi bali alipiga picha ile nyumba na gari kisha akageuza gari na kutembea.



    ANTANANATIVO-MADAGASCAR



    Ndani ya maabara kubwa ilimokuwa ikitegemewa kusukwa Bomu kubwa kabisa la kibaolojia, tayari mambo yalishaanza. Tereza aliyekuwa amebadilika kutoka kwenye kugoma kuto kufanya kitu chochote kile kuhusiana na utengenezaji wa sumu au bakteria mbaya atakaye waangamiza waafrika kwa wingi sana, sasa alikuwa ndani ya maabara hiyo tena kwenye mavazi maalumu kwa ajili ya kazi hiyo tu. Alikuwa ameshaanza kazi ya kuchemsha kemikali zake ajuazo yeye akichanganya na zile alizozikuta mahali hapo. Alikuwa haongei pia alikuwa kiziwi kabisa. Taarifa aliyoitoa Dokta Henry ni kwamba Tereza asingeweza kuongea kabisa pamoja na kusikia hadi anakufa au hadi mwisho wa maisha yake kwa maana nyingine. Alionekana kupata tatizo kubwa sana kwenye mifumo yake hiyo miwili.



    "Amepata tatizo kubwa sana kwenye ubongo wake, tatizo hilo limeharibu mfumo wa usikivu na uongeaji wake, tungeweza kumfanyia upasuaji angepona na kurudi kwenye hali yake ya kawaida" alikuwa akiongea dokta Henry alipokuwa akitoa taarifa hiyo.



    "Tutapoteza muda sana kama tutamfanyia upasuaji huyu, ilihali anafanya kazi yetu bila shida yoyote basi hakuna sababu ya kuijali afya yake" alijibu Dr. Lee kwa sauti yake ya kukoroma.



    "Lakini hajaathirika zaidi kwenye kumbukumbu huyu binti, asije akawa ameathirika akatutengenezea vitu vya ajabu!" alionesha mashaka yake Bencov pindi alipokuwa akizisikia ripoti hizo za kidaktari.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Hapana, kwenye kumbukumbu yuko vizuri, ninyi wenyewe ni mashahidi tulipompeleka mbele ya mwili wa baba yake, alikuwa akiumia sana lakini alikuwa hatoi sauti wala hakuwa akisikia tunachojadili pale, hii ilimaanisha kuwa anajua kila kitu lakini kuongea ndiyo anashindwa. Kama angekuwa ameathirika kwenye kumbukumbu basi asingemwaga machozi pale" ndivyo alivyokuwa akizidi kutoa ufafanuzi Dr. Henry.



    Madaktari wote walikuwa nje ya maabara ile aliyokuwa akifanyia kazi Dr. Tereza. Alikuwa hataki mtu mule ndani zaidi ya mabinti wawili wauguzi aliowachagua mwenyewe. Dr. Henry na jopo zima la madaktari wanaofanya kazi kwenye maabara hiyo, walikuwa wamekaa kwenye chumba cha mitambo wakifuatilia kila kitu kilichokuwa kikifanyika ndani ya maabara ile. Tereza alipokuwa akihitaji kitu huwa anaagiza kwa ishara tu na huwa hapendi kurudia mara nyingi, akikuambia kwa mara ya kwanza, pili, ukiwa hujamuelewa anafanya mwenyewe. Kazi ile ilikuwa ikienda kwa kasi sana hadi wote pale wakawa wanashangaa. Siku tatu zilikuwa zimeshakatika tayari tangu Tereza kuanza kazi hiyo mfululizo. Kila mtu mule ndani alikuwa na furaha kubwa sana kuona kuwa kilichobakia kilikuwa ni kitu kidogo sana cha kumalizia.



    "Kazi inakwenda vizuri na kwa kasi kubwa" alisema Dr. Henry akiwa kwenye kikao cha kupata chakula cha pamoja na mabosi wake. Muda huo walikuwa wamekwisha kupata chakula kizuri sasa walikuwa wakikisukumia chakula hicho kwa kinywaji safi chenye kilevi kikali.



    "Tunakila sababu ya kujipongeza hadi hapa tulipofikia" aliongea Dr. Lee.



    "Kweli kabisa mkuu lakini tusijiaminishe moja kwa moja" aliongea Bencov na Lady Devil akauliza kwa nini.



    "Waitwe wale mabinti wawili kisha wathibitishe ni hatua gani waliyofikia na ni wapi walipobakiza" wote wakatulia baada ya maneno hayo na kijana mmoja akatumwa kwa ajili ya kwenda kuwaita hao mabinti ambao walikuwa bega kwa bega na Dr. Tereza. Wakati hao mabinti wakiwa wanakwenda huko walipoitwa, Tereza alikuwa akiona kila kitu kwani alijifanya amejibanza mahali huku akijifanya kusoma kitabu fulani kikubwa cha kikemia lakini picha lote aliliona.



    "Nilijua tu kuwa mtawatumia hao kujua nafanya nini na nimewatumia hao makusudi ili muweze kuniamini zaidi" alisema hayo moyoni binti huyo. Manesi wale walifikishwa mbele ya mabosi zao kisha wakaambiwa waeleze hatua waliyofikia. Wale mabinti wakaeleza kila kitu wakijuacho wao na hatua waliyobakiza kuweza kumaliza bomu hilo baya. Vicheko vya ushindi vikasikika hata Bencov ambaye alikuwa hana imani na binti huyo akawa na imani naye.



    Usiku mnene wakati kila mtu akiwa amelala ndani ya jumba hilo. Tereza alikuwa akitoka kimaajabu sana pasipo wao wenyewe kujua. Ilikuwa ikitoka ile nafsi ya Tereza wa ajabu aliyekuwa akitembea pasipo kuyafumbua macho yake huku mwili ukiwa umelala haujitambui. Nafsi ile ilitumia muda mchache sana kuweza kufika kwenye lile jumba la ajabu lililopo katikati ya msitu, jumba la kutisha, jumba ambalo tangu kuliona kwake lilikuwa likisikika vilio mchanganyiko. Vilio vya watoto, wakina mama na wanaume. Hakukuwahi kusikika vicheko ndani ya jumba hilo la kutisha. Wakati Tereza nafsi, akiwa anaingia tu kwenye mlango wa jumba lile, Damu inzito ikawa inaibuka kutokea chini ya sakafu, ilikuwa ikipitia kwenye nyufa za sakafu hizo. Ilikuwa ni damu inzito sana na ilikuwa ikionekana bado mbichi kabisa yaani kama kulikuwa kuna mnyama au wanyama wakubwa walikuwa wakichinjwa muda huo. Kama ni wanyama, swali la kujiuliza je, hizo sauti za watu waliokuwa wakiomba msaada ni za nini? Baada ya zile sauti za vilio kukata, kukaanza kusikika kile kinanda ama nari ya ajabu, nari iliyokuwa inaleta ladha ya muziki wa taratibu sana na wenye kuhuzunisha. Tereza wa ajabu au Tereza nafsi, alikwenda kwenye mlango mmoja mkuukuu akaufungua lakini bado alikuwa yupo katika hali yake ileile ya kutokuona au kutazama. Ndani ya chumba kile kulikuwa na harufu kali sana na uliyokera kama ungepata kuinusa lakini kwa Tereza nafsi haikuwa hivyo, alikuwa yu katika sura ya tabasamu sana lakini si kuona anachokitabasamia.





    Alipofika ndani ya kile chumba Tereza nafsi alitulia kisha akaanza kulishika tumbo lake ambalo ndani ya chumba hichohicho alipandikizwa kitu cha ajabu sana. Akanyoosha mkono wake hadi juu ya kabati moja kuukuu akachukua kitu kwenye kijichupa kidogo sana kama cha PPF. Akakifumbata vizuri kisha akatoka kwa haraka sana huku ile ala ya muziki ikimsindikiza hadi alipofika mbali ya lile jumba na ile ala ikawa imepotea. Alishtuka kutoka usingizini Tereza akiwa anahema kwa nguvu sana, alikitazama kile chumba kwa macho ya mshangao mkubwa akaonekana kukishangaa zaidi mithili ya mtu aliyekuwa akijiuliza yuko wapi. Alipofungua kitanga chake cha mkono akakuta kijichupa kidogo sana kikiwa kimefungwa imara kabisa. Akafumba macho tena na alipokuja kuyafumbua alikuwa akitabasamu.



    Hiki ndicho kitu ambacho Dr. Lee, Bencov, Merina au Lady Devil na watu wake walikuwa hawakijui. Tereza yule wamjuao wao alikuwa si Tereza huyo wa sasa. Huyo alikuwa ni Tereza mpya kabisa aliyebeba siri mpya na nzito kabisa kifuani mwake. Tereza alikitazama kile chumba kwa macho makali, alitatazama kila kona ya chumba hicho kisha akanyanyuka na kukaa sakafuni. Alivuta chupa kadhaa kutoka kwenye uvungu wa kitanda na kuanza kufungua moja baada ya nyingine kisha kuichukua ile chupa mpya ambayo aliikuta kitangani mwake ambayo yeye mwenyewe alikuwa akiamini imekuja kwa njia ya ndoto pasipokujua kuwa nafsi yake ilikuwa ikifanya mawasiliano na viumbe wengine wa ajabu. Alikuwa akichanganya kimiminika kile kipya kwa kila chupa, alipohakikisha hakuna chupa iliyobakia, akafunga vizuri kila chupa na kuzirudisha kwenye chombo anachokitumia kuhifadhi kisha akarudisha kule uvunguni. Alikitazama tena kile chumba kama awali kisha akajinyanyua na kurudi tena kitandani kulala.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Picha tatu zenye ukubwa wa saizi, zilitupwa juu ya meza na Petii. Roi alizitazama zile picha kisha akauliza pasi na kuzitazama.

    "Za nini hizi?"

    "Zitazame kwanza kisha ndipo uulize, waafrika kwanini hambadiliki?" alijibu Petii. Roi akamtazama huyo binti kwa tuo kidogo kisha akataka kumwambia neno kutokana na kauli aliyoisema lakini hakupewa nafasi hiyo kwani huyo binti alikuwa ameshakiacha hicho chumba na kuelekea bafuni. Roi akaziinua zile picha na kuigeuza moja baada ya nyingine.

    "shit! Hii si ile gari niliyoiona kule kwenye nyumba ya Marehemu Ndungai? Huku nako?" aling'aka na kujiuliza maswali mchabango bila majibu.

    "Alikuwa nyuma yangu huyu binti" akajisemea kisha akaachia tabasamu na kuitazama ile nyumba vizuri akaihifadhi kwenye memori kadi ya kichwa chake. Akawa anamsubiri Petii tu ili ajue ni mtaa gani huo. Petii aliporudi, alikutana na swali hilo la kwanza kabla haja kaa chini.

    "ni pale pale mjini madukani, mtaa wa pili kabla hujavuka barabara ya Bank ya ujamaa nyumba ya tatu" alijibu vizuri tu Petii.

    "ok, pumzika tutaonana baadae"

    "nani kasema anabaki mtu hapa, unachokitafuta wewe hata mimi nakihitaji kwa faida ya kazi yangu, tunakwenda wote"

    "ok, follow me" aliongea Roi huku akiwa wa kwanza kutoka mule chumbani. Walikifunga chumba kile kwa utaalamu wa ujuao wao wenyewe kisha wakatoka pamoja hadi maegeshoni wakaingia kwenye gari anayoitumia Petii wakaondoka. Haukuwa mwendo mrefu sana kutoka hapo walipo hadi Madukani, ulikuwa ni mwendo mfupi sana. Waliegesha gari mbali kidogo na nyumba waliokusudia kwenda kisha wakatembea kwa miguu kwa umakini mkubwa hadi mahali ilipo nyumba hiyo. Roi akaonesha ishara kuwa yeye anatangulia ndani kisha Petii afuatie nyuma. Huyo binti alibana kwenye uzio wa michongoma hadi Roi alipofungua mlango kwa kutumia ufunguo usioshindwa na kitasa cha aina yoyote ile, ndipo binti huyo naye akafuatia. Waliufunga mlango kama walivyoukuta. Nyumba ilikuwa kimya sana kuashiria kuwa hakukuwa na mtu humo ndani. Roi alipotazama saa yake ilikuwa ni saa tano na dakika sita.

    "vipi?" wakaulizana.

    "zima hiyo taa kisha tumsubiri mwenyeji wetu, inavyoonekana atakuwa yuko kwenye ulabu, hebu tafuta mahali pa kukaa" aliongea Roi lakini wakati anafika tamati, kuna gari ilikuwa inaingia hapo kwenye hiyo nyumba.

    "Hajachelewa sana kaa tayari" aliongea Roi huku akiisikiliza hiyo gari. Ilikuwa haijazimwa kwa muda kidogo na baada ya dakika kama moja, gari hiyo iligeuzwa na kuondoka huku ikiacha sauti ya kilevi iliyokuwa ikijikokota kuukaribia mlango. Mtu huyo alikuwa akiimba nyimbo zisizoeleweka hata kidogo mara mlango ukatiwa ufunguo ukakubali, ukasukumwa pia ukakubali na msukumaji kuingia kwa fujo na kufuata swichi.

    "Maisha....maisha ni...nini, maisha ni matamu ukiwa na....na akili....tunakula, tunakunywa, tunavaa kwa aji.....kwa ajili ya pesa" alikuwa akiropoka huyo kijana. Alikuwa ni kijana mdogo sana mwenye mwili wa kawaida lakini ulioonekana si mwili wa kibwege, ulikuwa ukijua umuhimu wa mazoezi. Aliivuta fulana yake juu akaitoa lakini alipoitoa hiyo fulana, akashangaa kuna mtu alikuwa amekaa kwenye meza iliyopo hapo sebuleni.

    "Wewe ulikuwepo hapa au umekuja saa ngapi si ulise.....mh! Siye!" aliongea kwa ulevi lakini alipogundua kuwa aliyekuwa akimdhania siye, alibadilika ghafla, akaruka nyuma huku mkono wake ukikamata bastola iliyokuwa kiunoni mwake. Roi alibingilia kwa haraka sana kwani kasi ailiyoruka nayo nyuma huyo kijana hakuitegemea kabisa machoni mwake. Risasi moja ikavunja meza, inamaana Roi angechelewa tu angeisoma. Yule kijana akawa anaitafuta shabaha nyingine asiipate, Roi alibinjuka na kutulia nyuma ya kochi la kileo.

    "wewe ni nani?" aliuliza yule kijana kwa sauti ya kilevi lakini iliyotengemaa kidogo.

    "muulize huyo hapo nyuma kwanza kisha unigeukie na mimi" alijibu Roi makusudi kabisa kwa kujua kuwa huyo kijana na pombe alizokunywa, umakini lazima utakuwa umepungua. Kitendo cha huyo kijana kugeuza shingo, tayari Petii alishabinjuka kutokea nyuma ya kochi jingine la karibu. Mateke mawili mazito yakamrudisha nyuma huku ile bastola ikimtoka mikononi akiwa bado anaitamani. Petii hakumpa nafasi ya kujipanga, alimuadhibu kwa mapigo mawili ya nguvu hadi akatulia.

    "Nani aliyekutuma kule kwa Backa na kwa marehemu Ndungai?" Roi alitupia swali akiwa amekaa kwenye kochi la mbele yao tayari. Swali hilo likamfanya huyo kijana achachawe, hakujua hao watu ni wakina nani na wamejuaje kuwa alikuwa kule. Kila kitu alikifanya kwa umakini mkubwa sana na alihakikisha hakuna mtu aliyekuwa akimuona sasa hao ni kina nani.

    "Sijui hata kama nilikuwa huko, smjui hata mmoja kati ya uliowataja hapa" alijibu kwa jeuri Kijana huyo. Teke moja la tumbo kutoka kwa Petii lilimpa maumivu makali yaliyomfanya kujikunja sana.

    "Jibu ulichoulizwa sisi siyo wajinga kuja hapa. Hata sura yako inakusaliti mjinga wewe, hebu jibu kama unataka kubaki hai" aliongea Petii, huyo kijana alimtazama huyo binti kisha akacheka huku akitaka kujichoma kisu cha kifua kwa haraka sana. Hiyo ndiyo ilikuwa kanuni ya kazi yao, yaani ukiona umezidiwa na huna jinsi jiuwe kabla siri haijawa uchi. Petii alikiona hicho kisu akakipiga teke na kukitupilia mbali na kumtandika ngumi ya kwenye mfupa wa pua. Kelele za uchungu zikamtoka huyo kijana damu zikaanza kumtoka.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "hutaweza kujiuwa kama ndilo wazo lako, utaumia tu kama utazidi kuwa mkaidi, hebu niambie ni nani alikutuma" Roi mwenyewe alinyanyuka na kumchoma kisu cha paja huyo kijana huku akimtaka aseme. Kelele za maumivu zilikuwa kubwa sana. Roi alizidi kukizunguusha kile kisu pale kwenye paja.

    "Jasusi pekee ndiyo anaweza kuvumilia haya maumivu na akakubali kufa lakini asitoe siri si wewe" alizidi kuongea Roi huku kile kisu kikikaribia kuufikia mfupa wa upaja.

    "Aaaaaa Don Philipo,.....unaniumiza Shoga wewe!" alijibu huyo kijana huku akitoa ukelele mkali sana wa maumivu. Baada tu ya kutoa majibu yale Roi alikiacha kile kisu kwenye lile jeraha lililokuwa halitamaniki kwa damu kisha Petii alikikamata kile kisu akamkita cha kwenye moyo.

    "kufa kwa amani" alimsindikiza na hayo maneno kisha akamtazama Roi ambaye alikuwa amekasirika ghafla.

    "Ninashida na huyo Philipo" alisema Petii.

    "Utampataje sasa wakati wa kukupa muelekeo umeharakisha kumuuwa. Wanawake bwana papara tu ndiyo imewajaa, unadhani tutampataje huyo Philipo sasa.......!" Alikuwa amechukia sana kijana huyo juu ya kile alichokifanya Petii lakini wakati Roi akiwa anaongea kwa hasira mahali hapo, akakatishwa na muito wa simu ulionza kuita kutokea kwenye mifuko ya suruali ya huyo kijana. Petii akaitoa kisha akamtazama Roi usoni ambaye alimpa ishara kuwa asiipoke simu hiyo. Simu hiyo ikaita hadi ikakatika. muda mfupi ukaingia ujumbe. Petii akaufungua haraka sana.

    "Najua umelewa sana. Kesho asubuhi majira ya saa mbili tukutane P House, Don anatuhitaji" Roi akautazama huo ujumbe haukumsaidia kitu, akaitumbukiza simu mfukoni akiwa amefura na kuvuta hatua kutaka kuondoka. Mara ujumbe mwingine ukaingia, alipoufungua ujumbe huo akatabasamu.

    "hapana, saa mbili Don atakuwa na kikao na wakuu hivyo anahitaji tuonane wakati wa chakula cha mchana Pande New Hotel" hiki ndicho pekee kilichomfanya atabasamu. Kwani alijua kuwa kupitia ahadi hiyo ndiyo itakuwa mwanzo wa safari aitakayo. Wakaondoka.



    @@@@@



    "Wapi sasa natakiwa kuanza napo kati ya hapa na hapa?" alijiuliza kijana Bogo au waweza kumuita Inspekta Bogo. Alikuwa ametulia kwenye mgahawa mmoja uliopo pembezoni kidogo mwa ofisi za shirika moja la uma. Hakuwa akipata chakula wala nini, hamu ya kula haikuwepo kabisa kinywani mwake. Muda alikuwa akiusogeza mahali hapo kwa kujiburudisha na sharubati ya chungwa. Kazi ile ya kupeleleza kwa siri ilikuwa ikianza kumtumbukia nyongo kila hatua aliyokuwa akipiga, hakuona kama anafanya kitu.





    Kuna kitu aliwaza akiwa mahali hapo. Akatia mkono mfukoni akatoa kitabu chake kidogo cha kumbumbu kisha akapiga namba fulani mahali akaweka hiyo simu sikioni.

    "niambie kijana?" alisalimia, upande wa pili ukajibu kwa shangwe kubwa kisha ukauliza sababu za ukinywa alioupiga kwa kitambo kingi. Bogo akajibu.

    "Mambo yamekuwa magumu sana ndugu yangu, kila nikipiga hatua moja mbele, naona kama narudi nyuma" upande wa pili ukawa kimya kwa muda kidogo huku kukisikika michakacho mithili ya mtu anayevuta hatua kisha ukasema kuwa, alikuwa anatoka mbali kidogo na ofisi kwani hakuwa na imani na mtu na alijua kuwa simu hiyo hakumpigia bure, liko jambo.

    "ni kweli kijana liko jambo" akasema kisha akaendelea baada ya kuweka pozi kwa muda.

    "Ninakutumia namba ya simu sasa hivi nataka uifanyie kazi na uniambie ni ya nani na inasoma wapi kwa sasa maana sasa nataka kuingia ndani zaidi, si unajua tena ukitaka kumjua adui yako usimuogope" Baada ya kusema hayo, upande wa pili ukamtahadharisha umakini kwanza kisha akamwambia aitume hiyo namba na yeye ataifanyia kazi na kumpa majibu muda huohuo. Simu ikakatwa, Bogo akatuma namba alizozikusudia kisha akatulia kusikilizia majibu. baada ya kama dakika saba, simu yake ikaunguruma akaiweka haraka haraka sikioni.

    "hii namba ya simu umeipatia wapi Inspekta?" lilikuwa swali kutoka kwa mtu aliyemtambulisha kama kijana.

    "Kwanini umeniuliza hivyo Kijana?"

    "Imenishtua kidogo na kama huyu yumo kwenye mlolongo wa watu unaowapeleleza basi kazi si ndogo na sina hakika kama tutafikia lengo"

    "Sijakuelewa unamaanisha nini bado, unanizunguuka tu kijana bila kuniambia hiyo namba ni ya nani na nampataje?"

    "Unajua kwa nini nimekuuliza hivyo?"

    "Enhe!"

    "Jina la mmiliki wa namba hiyo ni Kijazi Zambion, si jina tu na picha yake pia nitakutumia baada ya maongezi haya. Namba hiyo kwa sasa iko hewani inaonekana yuko na maongezi na mtu. Namba hiyo inasomeka karibu tu na mahala ulipo mnara wa simu wa pale New Hotel, Town hapo kuelekea Pande New Hoteli" alizidi kueleza huyo kijana lakini pamoja na maelezo hayo yote, bado Inspekta Bogo alikuwa na swali alilolitakia majibu kutoka kwa Kijana huyo.

    "Kwani unamfahamu huyo mtu?" akauliza. Kijana akajibu.

    "Simfahamu sana kiundani ila huyu jamaa alishawahi kuwa mbunge kipindi cha Mh. Mobande alipokuwa madarakani lakini hakudumu sana akaachia ngazi kwa sababu zisizokuwa wazi, bwana huyo akabaki kuwa 'Partiner' mzuri na wa karibu sana wa Mobande akiwemo na Mlinzi wake wa karibu aliyekuwa akifahamika kwa jina la Kitema, huyu sijui mahali alipo kwa sasa" ndivyo alivyoeleza Kijana. Kimya kikachukua nafasi pumzi zikashuka kutoka kifuani mwa Inspekta Bogo akajua sasa anakaribia kuwa karibu na matukio makubwa.

    "Sasa inasomeka Pande New Hotel?" akauliza kisha akajibiwa ndiyo inasomeka hapo.

    "Ok, nashukuru sana kijana na nitakuwa nikikupigia kila nitakapohitaji msaada wako, kuwa makini sana na hao wafanyakazi wenzako kwani huu mchezo ni wa kutazamana usoni" akasema Insp. Bogo. Simu ikakatwa. Bogo alitoa noti mbili za shilingi elfu moja moja akazibana na ile gilasi ya sharubati ambayo aliipiga yote. Akatoka hapo na kuingia garini mwake safari ya kuifuata Pande New Hotel ikaanza. Hao ndiwo vijana wa IGP Liyambo ambao aliwaweka maalumu kwa ajili ya kutegemeana. Huyo aliyefahamika kwa jina la kijana alikuwapo kwenye ofisi fulani kwa ajili ya kazi kama hizo za siri.



    Roi alikuwa ndani ya ile Hoteli akiwa amefika muda wa saa moja nyuma, hiyo ilikuwa ikimaanisha kuwa alitangulia kabla ya waheshimiwa hao wa miadi kukutania hapo. Mbele yake kulikuwa na meza kubwa ya kutosha watu watatu lakini alikuwa peke yake huku meza hiyo ya duara dufu ikipendezeshwa na chupa moja safi ya bia ya kimea halisi cha Taifa hilo. Macho yake hayakuchoka kutazama mlangoni huku yakim-note kila anayeingia na kutoka. Macho hayo yalikuwa ndani ya mawani ya giza hivyo ilikuwa ni vigumu sana kuweza kuona kama unatazamwa naye. Baada ya lisaa hilo limoja kupita, wakaingia watu wawili humo ndani, wote walikuwa ndani ya suti safi kabisa zilizokuwa zikinyurutika fedha kuanzia suruali hadi koti, ilionesha dhahiri kuwa suti hizo hazikuwa zao au malighafi ya Taifa hilo. Bila shaka zilitoka kwenye viwanda vya huko duniani. Walikuwa wakicheka watu hao huku wakionekana kuwa siriazi sana kwenye maongezi hayo. Wakachagua mahala pazuri pa kuweka kituo. Ilikuwa ni pembeni kabisa kwenye dirisha kubwa ambalo lilikuwa likiwapa fursa ya kuona mahali walipoegesha magari yao ya gharama. Muhudu hakusita kuitenda kazi yake, alisogea hadi kwa mabosi wale kuuliza mahitaji.

    "Subiri kidogo binti tutakuhitaji baada ya muda mfupi, kuna watu tunawasubiri na tuko kwenye maongezi" alijibu mtu mmoja mwenye mashavu makubwa na macho makubwa kiasi huku akionekana si mtu wa kucheka au kutabasamu mara kwa mara. Sura yake haikuwa hivyo, haikushabihiana na kicheko wala tabasamu. Bwana huyo mwenye mashavu makubwa, akatoa sigara kubwa la kimarekani (Sigger) akaliweka kinywani mwake na kuiwasha. Wakaendelea na maongezi.

    "nipe habari bwana mkubwa, maisha unayaonaje kwa sasa na biashara zako?" akaongea mmoja kati ya wale mabosi.

    "Maisha sidhani kama yanashida hasa ukiyapatia, anayekwambia maisha magumu ujue huyo ni mwoga wa fikira zake mwenyewe. Unajua fikira ukizifikirisha zinakupa manufaa lakini ukizipa hofu na unyumbu, lazima maisha uyaone magumu" aliongea bwana Kijazi, aliongea kwa majivuni makubwa sana huku mikono ikiwa haitulii mahala pamoja, nayo ilikuwa ikitoa nasaha za kivitendo pale maneno ya kibosi ya bwana huyo yatokapo.

    "Ni kweli kabisa usemayo?" alikazia Philipo au Don Philipo kama vijana wake wanavyomtukuza. Wakati wakiwa wanazidi kupepeta domo mahali pale, macho ya Roi kama kawaida yakapokea mgeni mwingine mmoja. Huyu alikuwa tofauti kidogo, aliingia kwa utaratibu sana lakini utaratibu wake ulikuwa na jambo ambalo kwa mtu makini kama Roi alijenga picha fulani. Mtu huyo hakumfuatilia sana kwani muda huo huo kukaingia watu wengine wawili, hawa ndiwo waliomshughulisha kwani walisogea kwenye meza ya wale mabwana wenye kila hali ya ubwana mkubwa, wakaketi kwenye nafasi mbili zilizokuwa wazi. Kijazi aliizunguusha shingo yake kila kona mule ndani na muda mfupi tu muhudu alikuja.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Uko makini sana na kazi yako, haya hebu hudumia kwa kila mmoja hapa" alisema Kijazi kisha kila mmoja pale akachagua kinywaji akipendacho huku yeye akiagiza maji.

    "Kabla hamjatuacha hapa kwa ajili ya kumalizia maongezi yetu mliyotukuta nayo, kwanza mnipe taarifa ya kila mmoja wenu ni wapi mmefikia na ni yapi mafanikio" alisema Don Philipo huku akiwatazama kwa nafasi kila kijana hapo.

    "Mimi kwa upande wangu sijafeli, nimeweza kujua nyendo na mipango ya Tamimu. Anaonekana yuko anashughulika na biashara zake haonekani kuwa na mpango na kufuatilia kifo cha baba yake tena. Anazidi kuhakikisha kampuni yake ya magari inazidi kukuwa" alieleza kijana mmoja hapo.

    "Well done!" alijibu Don Phili, akasema.

    "Pamoja na hayo lakini tutazidi kumfuatilia ili tujue ni kweli ameridhika na kifo cha baba yake na hatofuatilia kitu hicho, kisha tukijua hapo ndipo tutakapokuwa na la kuamua" akamgeukia na kijana mwingine ili kujua alipofikia na yeye.

    "Kwa upande wangu bado sijaona kitu kipya, hakuna harakati zozote ambazo IGP anazifanya kuhusiana na ufuatiliaji wa kesi zile. Inaonesha vitisho vyetu kwao vimeweza kuzaa matunda mengi sana kwani kila nikimuuliza mtu wangu niliyemuweka kwenye ofisi yake kuu, ananiambia kuwa mkuu wake amepoa sana na hakuna hatua za hatari kwetu anazobuni" alijibu huyo kijana. Philipo akasema kuwa hapo wasibweteke kwani mambo ya serikali anayajua pia anajua hakuna watu wabishi kama polisi. Kitu kimoja kikawa kinawatatiza na hawakujua nini kimetokea.

    "Inavyoonekana hamkumpa taarifa Mwenzenu si ndiyo? Mbona hadi muda huu hajatokea hapa?" aliuliza Don Philipo huku sura yake ikianza kubadili rangi kutoka kwenye weupe aliobarikiwa na Mungu hadi kuwa mwekundu, hizo zilikuwa ni hasira tayari.

    "Hakuna kitu ambacho sikipendi kwenye kazi kama uzembe, vijana wako wanaonekana ni mahodari sana wa kufanya kazi kwa wakati lakini wanasumbuliwa na vimelea vya uzembe" aliongea Kijazi. Maneno yake yakampandisha hasira Don Philipo akaanza kuonekana kuchukia zaidi.

    "Hakikisheni huyu mwenzenu anamipa taarifa kuwa yuko wapi haraka, nataka kujua kuhusu yeye kwani nilimpa kazi muhimu sana yule hivyo sitaki ujinga...mkileta ujinga nakwenda kufuta yale mema mliyoyafanya kwangu na mtaumia" alifoka sana Philipo lakini hakuwa akiongea kwa sauti kubwa, hakutaka kumpa faida kila mmoja aliyeko pale. Pamoja na hayo yote hawakujua kama kulikuwa na kiumbe au viumbe wawili waliokuwa wakifuatilia maongezi yao.

    "Don, simu ya Romy haipatikani hewani!" alijibu kijana mmoja mara baada ya kuishusha simu mezani. Alikuwa akitetemeka sana kwa hofu.

    "Romy asilete ujinga na mimi kabisa, Romy atakufa, hebu msiniambie hapatikani nataka taarifa zake sasa hivi" aliwaka Don Philipo. Kijana mmoja akainua simu na kupiga mahali.

    "Sebastian naomba ingia kwa Romy hapo mcheki na unipe jibu sasa hivi, sikati simu nasubiri jibu" kijana huyo baada ya kutoa maagizo hayo akatulia kimya kusubiri.

    "What!.....Nini wewe, kweli...aaaaah!" alihamaki huyo kijana huku macho yakimtoka pima simu hiyo badala ya kukata alijikuta akiizima kabisa kwa mchecheto alioupata. Taarifa aliyoipata kutoka kwenye simu hiyo haikuwa ile waliyoitarajia kabisa.

    "Don, Romy amepoteza maisha!"

    "Unasemaje wewe...kivipi sasa?" alishangaa sana Don Philipo, habari ile ilikuwa mbaya sana kwake. Amekufajekufaje? likawa ndilo swali lililokuwa likimzunguuka kichwani mwake.

    "Amechomwa kisu cha kifua akiwa sebuleni kwake" alisema huyo kijana.





    . Kisu, kafa kwa kuchomwa kisu? Ah aha! Aliwaza Don Philipo, hakuamini ile kauli.

    "Eti, Romy kafa kwa kuchomwa kisu, umesikia Kijazi?" aliuliza swali la kuchanganyikiwa Don. Kijazi hakujibu alikaa kimya tena kimya kikuu huku kichwani akiwa na maswali kibao aliyokuwa akijiuliza. Kama kijana wao kauwawa ni wazi kutakuwa na kiumbe anafuata nyayo zao. Huyo kiumbe ni nani sasa. Hayo ndiyo yaliyokuwa yakimfikirisha Kijazi muda huo. Macho yake yalishajifinya ndani kwa ndani, hii ilimaanisha kuwa hakuwa na furaha tena, kuna kiumbe hatari au anayeanza uchokozi mahali pasipochokozwa alikuwa akija kwao. Alivitazama vitanga vya mikono yake kwa muda akakumbuka siku ya mwisho kufanya mauwaji na viungo vyake hivyo. Akakumbuka ni siku anauwa wapelelezi wale wawili wa Tanzania. Kumbe huyu ndiye aliyesuka ule mpango wa ajali ya wale wapelelezi kisha kummalizia yule mpelelezi mmoja kwa risasi baada ya kugundua mmoja amefia palepale. Kifo kingine ni siku anamuuwa Mr. Ndungai nyumbani kwake.

    "Ninamasiku kibao sijauwa" akajisemea kisha akanyanyuka, ndivyo alivyo huyo bwana akikasirika basi ujue mtafute dawa ya kupoza hasira zake laa sivyo ni shida. Na hapo alikuwa anasubiri kitu atakachopata kwenye hicho atakachoagiza hapo kama kitakuwa hakimpendezei basi anazifikisha taarifa hizo kwa wakubwa zaidi yake.

    "Hakikisha mnamjua muuwaji, Don Philipo, nataka uwapange vijana wako au hata wewe mwenyewe mniletee sura ya huyo muuwaji anaejaribu kunusa nyendo zetu akiwa kafa" aliagiza hivyo kisha akakiuwa hicho kikao kwa mtindo huo wa pekee kabisa. Don Philipo akabaki ametumbuliana macho na vijana wake hao wawili.

    "Hebu tawanyikeni na jioni mniletee angalau kichwa tu cha huyo mshenzi ili nimridhishe huyu jamaa, hana mana huyu kama nikileta uzembe" aliongea kwa ghadhabu kuu Don. Wale vijana wakatawanyika.



    Inspekta Bogo alikuwa palepale akiwafuatilia wale mabwana na yeye tageti yake kubwa ilikuwa ni yule ambaye alikuwa akifuatilia nyendo zake kupitia simu baada ya kuzipata mahali fulani fulani kisha kuzifanyia upekuzi kupitia kijana makini aliyechomekwa kwenye moja ya kampuni ya mitandao ya simu. Huyo ndiye aliyekuwa fukununu au mfukuzi wa ufukuzi wa mambo siri. Lakini kutokana na hali aliyoiona pale japo yale maongezi hakuyasikia lakini picha aliiona kuwa huyo bwana anayekwenda kwa jina la Kijazi hakuwa mtu mdogo hivyo ni bora hata amfuatilie yule mwingine ambaye alikuwa hamfahamu jina ambaye kimavazi alikuwa akishabihiana na Kijazi.

    "Nani unashida naye kati ya hao waliotoka hapo nje?" aliuliza Roi baada ya wote pale ndani kutoka. Alikuwa akimuuliza Petii ambaye alikuwa nje ya ile Hoteli ndani ya gari akifuatilia kila anayeingia na kutoka.

    "huyu mwenye suti nyeusi ambaye nilikuwa sijui nitampatia wapi, sura yake nimeikumbuka baada ya kumuona" alijibu Petii.

    "Anaitwa Don Philipo au Don Phili"CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Ndiyo mwenyewe, mimi namfahamu kwa jina la Philipo" alijibu Petii, muda huo Roi akafika na kumpatia kadi ndogo mfano wa kadi ya biashara huku akimtahadharisha kuwa awe makini juu ya kadi ile. Ilikuwa inabendera ya Tanzania kwa pande zote mbili.

    "hakikisha unakuwa makini zaidi, sitaki wajue sisi ni akina nani bali wajue kuwa ni kiumbe kutokea Tanzania ndiyo aliyeyafanya haya" alisema Roi.

    "Kwanini sasa, hujui kuwa Nchi yangu ya Malawi imenituma kuja kuwaangamiza watu hawa na nilikuambia hivyo?"

    "Najua sana ila nafanya hivi kukuweka mbali na uhasama na vita hii, nilipokuja nimefanya uchunguzi wangu nimegundua kuwa watu unaowatafuta wewe ndiyo ninaowatafuta mimi. Mtandao huu ni mkubwa unavyoonekana, hivyo....Oooh! fanya nilovyokuelekeza, gari ya Don inaondoka now. Nitakuja kukuelekeza kila kitu baadaye ila tu, hakikisha hiyo kadi inakuwa kwenye mwili wa huyo marehemu, acha niifuate gari waliopanda hao vijana" alikuwa akitoa maelezo Roi lakini akakatisha kutokana na kuona gari ya Don ikitoka maegeshoni. Roi alitoka pale kwenye ile gari ubavuni mwa mlango wa dereva alipokuwa amesimama kisha akaingia kwenye gari moja aliyoikuta hapo ambayo si yake ila alitaka kuitumia kwa kazi yake kutokana na gari waliyokuja nayo kutumiwa na Petii kumfuatilia Don Philipo.





    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog