Search This Blog

Sunday 22 May 2022

HATI FEKI - 5

 





    Simulizi : Hati Feki

    Sehemu Ya Tano (5)



    *** *** *** ***



    MAX mara moja alifika eneo la maliwato kumsubiri Steve aingie. Aliwasiliana na John ili aweze kuzuia watu kuingia eneo hilo na badala yake awashauri watumie maliwato nyingine. Wakati huo hakukuwa na watu wakiingia maliwatoni huko na hivyo ilikuwa ni nafasi nzuri ya Max na John kufanikisha mpango wao.



    Haikuchukua muda Bosi Steve aliingia, Max alisubiri hadi amemaliza na kuchomoa bastola yake na kumnyooshea Steve. Bosi Steve alishtuka kusikia sauti ya Max ikimwambia.



    “Usijiguse na simama hapo hapo kama ulivyo,” kabla ya kugeuka kumwangalia aliyetoa sauti hiyo alipigwa ngumi na kuzirai. Max aliwasiliana na John kwamba kashamteka hivyo wajitayarishe kuondoka.



    Antony alifungua mlango wa gari na kulisogeza mpaka karibu na mlango wa kutokea na hivyo ilimchukua Max dakika mbili kumfikisha Steve ndani ya gari hali ya kuwa amezirai.



    Walifika katika nyumba moja kuukuu iliyoko maeneo ya Mianzini wakiwa wameshamteka Bosi Steve. Nyumba hiyo haikuwa inatumiwa na mtu yeyote. Ilikuwa ni saa moja na nusu usiku.

    Baada ya Steve kuzinduka John alikuwa amesimama mbele yake. Alishtuka kumwona John.



    *****

    Ukumbini Mosses Ndula na Askari wake walikuwa wakimtafuta Bosi Steve bila ya mafanikio. Waliamua kutoka na kuelekea nje ya ukumbi wakidhani atakuwa huko kwani hata simu yake haikupatikana. Walizunguka kila mahali nje ya hoteli wakijua labda anavuta sigara sehemu.



    “Atakuwa ametekwa, hivyo wasiliana na kikosi cha anga ili kuzunguka na helikopta kujua watekaji,” Mosses Ndula alimwambia mmoja wa askarti wake ili aweze kuwasiliana na askari wa kikosi cha anga waanze kazi ya kumtafuta Bosi Steve mara moja.



    Mosses alijua lazima ni John kafanya mpango huo baada ya kufanikiwa kuwatoroka askari wake.



    “Huyu lazima atakuwa ni John na Aminata….Lazima tuwafuatilie,” aliwaza Mosses huku akiingia ndani ya gari.



    Max alishauri wampeleke Steve kwenye vyombo vya sheria ili akadhibitiwe huko wakati wao watakapokuwa wakiendelea na zoezi zima la kuivamia ngome yake na kuiteketeza. John aliafikiana na Max na hivyo waliongozana na magari matatu ili kuhakikisha wanamfikisha salama Steve.



    Wakiwa njiani kuelekea maeneo ya mjini kati waliona helikopta ikiwazunguka na kuanza kuwatupia risasi. Ni katika barabara ya Moshi Arusha ambapo kina John walikuwa wakielekea kituo cha polisi ili kumshikilia Steve.



    “Max jamaa washatuona tutoke tupambane nao, naona wanataka kuzima huu mpango, ni nani kawaambia tumepitia njia hii”? aliuliza John huku akitoa bunduki yake na kuanza kushambulia helikopta ya askari wa Mosses Ndula iliyokuwa ikiwalenga kwa risasi.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Max na John walijitahidi kurudisha mashambulizi. Waliteremka askari wa Mosses Ndula kutoka katika helikopta na kuvamia gari lililokuwa limembeba Bosi Steve na hivyo kufanikiwa kuzima zoezi la kina John la kumpeleka kituo cha polisi. Walifunga barabara na kuzuia gari lililokuwa limembeba Steve. Walifanikiwa kumchukua na kuondoka naye.



    “Aaah, hawa jamaa wametuziidi ujanja. Sijui imekuaje… sikutegemea itakuwa hivi isitoshe hatukubeba silaha za maana. Itabidi sasa tujipange upya,” alisema John kwa hasira huku akiiangalia ile helikopta ya Mosses ikitokomea angani.



    John na Max waliamua kurudi nyumbani kwa ajili ya kujipanga upya. Walimpigia simu Antony na kumjulisha ya kwamba watakutana tena baada ya kuwa wameshapajua.

    John alimpigia siu Aminata na kumjulisha ya kwamba mambo hayakuwa mazuri na hivyo wameamua kurudi nyumbani na kuanza upya mipango yao.



    Katikan jumba la Steve, Mosses anazidi kuchanganyikiwa, anawaita watu wake ili kujipanga kwa ajili ya mapambano. Steve aliyekuwa amekaa tu katika kiti kilichokuwa karibu yake hakuongea lolote. Alikumbuka alivyoambiwa na Mosses kwamba asindikizwe ila yeye alikataa.



    “Wale washenzi wameshaanza, sasa tusiwakawize. Tuhakikisheni tunawatokomeza,” Mosses alisema hayo huku Steve akitingisha kichwa kukubaliana naye. Amempa majukumu yote Mosses ya kuongea na kutoa amri kwa vikosi vyake na hivyo lolote litakalotokea Mosses ndiye alikuwa mwenye amri zote.



    Alikutana na Mosses wakati Mosses alipokuwa akiunganisha watu wake kwa ajili ya kuanza shughuli za mgodi ambao aliuchukua kwa Mzee Amigolas. Urafiki wao ulizidi kuwa mkubwa kwani walisaidiana kutafuta wanunuzi wa madini nje ya nchi pamoja na kushirikiana katika usafirishaji.



    Hali ilipokuwa mbaya kwa Mosses, Steve alijua na hivyo aliamua kumtafuta kwani mbali na kuwa akijishughulisha na mgodi, alijua kwamba Mosses alikuwa akijishughulisha na biashara nyingine pamoja na kujulikana na watu wengi maarufu na hivyo alijua akiwa naye ataweza kufanikisha biashara zake. Hivyo alimchukua na kuwa naye kama msaidizi wake katika kupanga na kuamua mambo ya kibiashara na kutafuta madili mengine yoyote. Pia katika kuiimarisha gome yake kwa kuongeza vikosi ambavyo vingedhibiti hali ya wasiwasi ambayo ingeweza kuikumba ngome yake.



    Mosses kwa kuwa alikuwa hana la kufanya baada ya kufilisika pale alipotoroka, sasa anakubali kuungana naye. Anataka kuwamaliza kabisa Aminata na John. Zoezi lake la kwanza alishindwa kutokana na askari wake kuzidiwa nguvu na hivyo anaamua kuanza msako wa kuwakamata na kuwaua peke yake.



    “Sihitaji mtu yeyote awaue John na Aminata…. Kazi hiyo nitaifanya mimi,” alisema Mosses huku akiitikiwa na Steve aliyekuwa akimsikiliza pamoja na vikosi vyake.



    “Tunaanza kazi sasa hivi, popote walipo watafutwe na waletwe hapa.



    Askari wote walitawanyika na kuwaacha Mosses pamoja na Steve. Waliingia ndani ya chumba cha silaha na kuanza kuangalia moja moja. Walichukua zile ambazo alijua zitawafaa na kutoka.



    “Tusipokuwa makini hawa jamaa watatuharibia mipango yetu. Inabidi tusimame imara. Hata kama wale wanaongozwa na serikali. Kwanza nitaongea na waziri wa ulinzi ili awapunguze nguvu,” Steve alisema huku akifikiria kuongea na Waziri wa Ulinzi ili awazuie askari wake waliotumwa kuja kuvuruga mippango yake.

    Alimpigia simu na kuongea naye baada ya kurudi katika ofisi yake.



    Alikuwa akisikilizwa na Mosses ambaye hawakuachana. Simu yake kwa waziri wa ulinzi ilikuwa ni kwa ajili ya kuzima mipango ambayo alikuwa hajaelewa dhamira yake.



    Waziri wa ulinzi walifahamiana. Hivyo baada ya kumsihi, waziri wa ulinzi alimwahidi kufanya vile alivyotaka. Aliita wakuu wa polisi na kuwaeleza juu ya hali inayotakiwa kuwepo. Mpango huo haukuwaingia John na Max ambao walikuwa pia ndani ya mkutano huo ulioitishwa na waziri wa ulinzi.



    Aminata ambaye alikuwa pia katika mkutano huo. Alifahamu kuwa hiyo ilikuwa imepangwa. Wakiwa wanamsikiliza waziri wa ulinzi, walikonyezana na kuamua kutoka nje.



    “Huyu waziri naona ana mawasiliano na wale watu, kwa nini atoe kauli kama zile? Huku ni kuzima mipango yetu.



    “Itabidi tuanze na huyo waziri….nani sasa atakayemzuia?”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hapana, tutamzuia kwa kuwasambaratisha wale wapuuzi. Tuhakikishe kwanza wale watu hawafanikiwi, kama waziri anajinufaisha kupitia kwao, sasa tukiwazima hatoweza. Na tutamfatilia pia. Tukipata hata picha yao ya pamoja tutahakikisha anawajibika baada ya mpango wetu kufanikiwa,” Max alisema huku John, Aminata na Antony wakimsikiliza na kukubaliana naye juu ya mipango yao.



    “Nadhani tuondokeni,” John alisema.



    “Hapana, tazameni kule…. Wamekutana naye… naona wanampongeza kwa kauli yake aliyoitoa. Sasa tusiwape nafasi. Hakikisheni hawawaoni na kila mmoja aondoke eneo hili tutakutana kesho kwangu,” Max alimalizia kusema huku kila mmoja akiingia ndani ya gari lake tayari kwa kurejea nyumbani na kukutana siku inayofuata kama walivyopanga.





    *****

    Mosses anaamini tayari mpango wa Aminata na John ambao anaamini wametumwa na serikali umeshazimwa. Hasira zinamkabili kila awakumbukapo. Anahisi bado wataendelea kumwandama kama ilivyokuwa kwenye mpango wake wa mgodi.



    “Sitaacha kuwatafuta hadi nihakikishe nawasambaratisha….washenzi wale walizima mpango wangu mkubwa sana…. mimi sio wa kuajiriwa… tayari nilishamiliki mgodi na kuwa mtu mkubwa sana,” aliwaza Mosses huku akiwa ameshikilia sigara yake ambayo ilikuwa ikiteketea taratibu katikati ya vidole vyake. Aliifuata chupa ya mvinyo na kuweka kidogo na kuibwia yote.



    Sasa aliondoka na kuufungua mlango kwa nguvu. Alimkuta Steve amesimama akimsubiri.



    “Nilikuja kukuchungulia. Ulikuwa unawaza sana. Nini zaidi ndugu?” aliuliza Steve kauli ambayo ilimshtua sana Mosses ambaye aliamini kwamba hakuna mtu yeyote aliyemwona alipokuwa amesimama. Alienda hadi pale alipokuwa Steve.



    “Hakuna baya mkuu….ni hawa washenzi wawili… sitamani wawepo duniani… nataka nihakikishe wanatokomea kabisa katika ulimwengu huu.”



    “Tuma askari wakawatafute bana….usiwaze na uwezo tunao. Waambie sasa hivi waanze msako. Watu wale hawawezi kutusumbua sisi.”



    Mosses alifanya kama alivyoambiwa na Steve. Aliwatuma askari kumi kwenda kuwatafuta na kuwakamata Aminata pamoja na John.



    “Ndio mkuu,” waliondoka kwa pamoja na kwenda kuchukua gari moja tayari kwa kuwatafuta na kuwapata John na Aminata kama walivyotumwa.



    *****

    Wakiwa ndani ya gari la Max, ulikuwa ni usiku saa tatu. Walikuwa wakirudi kutoka kikao kilichowahusisha wapelelezi wa Mkoa wa Arusha na Mwenyekiti wao wa upelelezi kilichofanyika katika hoteli ya Ngurdoto.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Aminata ambaye ndiye alikuwa akiendesha gari, aliyaona magari mawili yaliyokuwa yamesimama na kufichwa ndani ya kichaka. Alibaki akiwa anayaangalia tu huku akipunguza mwendo wa gari. Aliyashangaa yalivyokuwa yamesimama pasipo kuona mtu yeyote.



    Ghafla gari moja lilitoka na kusimama mbele yao na askari wengine wakitoka vichakani na kuwaelekezea bunduki zao. Wote walishtuka na ghafla walipunguza mwendo na kusimama. Walichomoa bastola zao na kuziweka tayari.



    Haikuwa kazi rahisi kama walivyofikiria kwani walishajua wale ni askari wa Mosses. John alitoa bastola yake na kuanza kuwatupia risasi. Aminata na Max nao walianza kuwashambulia huku Aminata akiongeza mwendo kulipita lile gari lililokuwa mbele yao.



    Max alilishambulia na kufanikiwa kumuua dereva wake baada ya kuwamaliza wale waliokuwa wamejificha vichakani. Lile gari lilienda na kugonga mti kisha kusimama. Haraka John na max walitoka na kuwafuata. Waliwaua wote na kuwaacha hapo hapo na kisha kuondoka.



    “Jamani mnaona,” alisema Aminata aliyeonekana kupatwa na wasiwasi.



    “Usiogope… sasa wamechokoza.” Alisema John.



    “Watajua tu watu wao wameuliwa na watajua lazima ni sisi. Sasa tusirudini home sasa hivi. Tutafuteni mahali tujiweke sawa alafu tuende. Zana zote zipo kwenye buti ya gari nlilompa Antony na mabegi mengine yapo kwangu. Tuyafuateni kwanza.”



    “Mi nadhani tungeekwenda hukohuko Mererani tukavamie kabisa. Hapo tutakuwa hatujawapa nafasi, kabla hawajajua kama watu wao wamekufa,” Max alitoa wazo ambalo lilikubaliwa na kila mmoja.



    “Lakini…. Nadhani tuwasiliane na Antony kwanza… yeye ndo anapajua.



    “Kweli, mpigie simu mwambia aje kamili. Aje usiku huuhuu, mwagize apitie kwangu Michelle atampa yale mabegi aje nayo,” alisema Max.



    John alitoa simu yake na kuanza kuongea na Antony.



    “Tayari nipo huku. Nyie njooni tu huku.”



    “Haa! Ok, sisi ndo tunageuza, uko kwa wapi. Na vipi mabegi tuliyoyapeleka kwa Max.”



    “Nliyaweka yote kwenye gari lake kabla hatujaachana nyie mkaenda kwenye kikao. Mimi nipo kwenye hoteli tuliyofikia kipindi kile. Nimefanikiwa kuingia hadi ndani na kutoka.”



    “Ndani wapi Antony?” alihoji kwa mshangao John.



    “Katika lile jumba lao. Nimeshapaona vizuri.”



    “Ilikuajekuaje kaka. Ngoja tuje afu utatuelezea poa,” John alimkatisha Antony asiendelee kuzungumza ili wafike kwanza.



    Antony alikuwa tayari ameshafika Mererani. Alifanya juhudi zote ili kuhakikisha anafanikiwa kuingia ndani ya lile jumba ambalo lilikuwa limefichwa. Jumba lililomilikiwa na Steve.



    Alifanikiwa kumrubuni askari mmoja wa Mosses na kumteka kisha kumuua na kuchukua mavazi yake. Alijichanganya na kufanikiwa kuingia. Alifanya kama walivyokua wakifanya wao na hivyo asingeweza kujulikana mapema kutokana na kufanana nao.



    Alifanikiwa kutoka na kurudi katika chumba chake alichopanga katika hoteli moja maarufu ambayo waliitumia wakati wa mashambulizi dhidi ya Mosses.





    *****



    Saa tano usiku kina John walikuwa wameshafika na kuungana na Antony. Walimkuta akiwa amevalia zile sare za askari wa Mosses.



    “Haah! Vipi tena Antony…umetusaliti nini?” aliuliza John huku akimkagua Antony na kuingia hadi ndani.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hapana….kwa hali ilivyo sidhani kama kuna kupumzika….viongozi wao wote wametoka. Kama mtakuwa mmesikia helikopta.

    Wametumia helikopta. Sasa tusizubae kabisa.”



    “Sawa tuanze na hao vibaraka wao.”



    “Usiku huu huu?” alihoji Aminata.



    “Ndiyo… kesho asubuhi watahadithia,” Antony alisema. John na Max walicheka.



    “Sasa sikilizeni, kutokana na nlichokiona ndani kule… nadhani sio pa kuchanganya. Mimi nitaanza kuingia nao alafu nitaacha mlango wa kuingilia ndani wa upande wa nyuma ukiwa wazi. Nyie mtapitia huko. Mkifika ndani mtakuta mi nimeshasambaratisha baadhi yao.”



    “Kweli,” aliitikia John aliyeonekana kuwa na shauku ya kupambana. Aminata alimwangalia na kutabasamu akikumbuka walivyoweza kupambana nao walivyokuwa wakidai mgodi wao.



    Alimwangalia zaidi na kumkumbuka mtoto wao ambaye hakujua lolote lililokuwa likiendelea. Alikumbuka pia John alivyomwambia abaki asiende kwenye mapambano ili mtoto wake asije akakosa uangalizi.



    “Mimi nitawasubiri hapa hotelini na nikiona mmezidiwa nitawasiliana na vikosi vyetu waje,” alisema Aminata. Kauli yake iliwashtua wote.



    “Hakuna tatizo, naamini sisi watatu tutaweza. Hakuna kumwonea huruma hata mmoja. Ni kuwaangamiza wote,” John alisema huku akiikoki bunduki yake na kuifunga vizuri. Max naye lifanya vivyo hivyo. Antony yeye allikuwa tayari amejikamilisha. Bunduki mbili nyuma ya mgongo na bastola iliyojaa risasi pamoja na mabomu mawili ya kurusha kwa mkono.



    John alimwangalia na kukumbuka mazoezi aliyokuwa akiyafanya. Anakumbuka pia alivyorudi nyumbani wakati baba yao alivyokuwa hai. Antony alitoroka katika mafunzo ya kijeshi aliyokuwa akifanyia katika kikosi kilichokua na kambi yake Monduli.



    Alikuwa amebakiza miezi michache tu amalize mafunzo yake ya kijeshi. Mzee Amigolas alikuwa amefanikiwa sana. hapo pakawa pamemchanganya Antony na hivyo aliamua aachane na kutumikia jeshi na kuamua kuwa karibu na baba yake. Miaka michache baadaye aliweza kupewa na baba yake miradi ya kusimamia ambayo ilikuwa Nairobi nchini Kenya.



    Alikuwa akiwasiliana na mmoja wa wanajeshi ambaye alimtumia ili aweze kupata vifaa vya kijeshi. Alifanikiwa kuvipata na hivyo kuvihifadhi tayari kwa mapambano na hivyo aliamua kwenda mwenyewe Mererani ili kufahamu zaidi kuhusu jumba hilo.



    “Naona umeshiba tayari kwa mapambano,” John alimwambia Antony huku akimpigapiga begani.



    “Niko tayari, sijui nyinyi kama mko tayari tutoke.”





    “Nadhani kwa wakati huu ulinzi utakuwa umeimarishwa sana….watatuona. sasa kwa nini tusiteke moja ya magari yao alafu tusogee nalo kabla Antony hajaingia nalo,” John alitoa wazo ambalo liliwafanya Anthony na Max wajilize kama wameafiki.



    “Kweli… antony itabidi uwazuie wewe ambaye umevaa sare zao alafu na sisi itabidi tukisha wateka na kuwaua tuchukue nguo zao tuingie nazo,” alisema Max na kukubalika kwa wote.



    “Kweli… tena naskia gari zinapita…. Antony toka ukacheki moja ulisimamishe.”



    Antony alitoka na kufanikiwa kusimamisha gari moja ambalo lilikuwa lina watu watatu. Magari mengine yaliendelea kwenda wakati yeye akiwa amelisimamisha lile moja. Hawakumwelewa. Walibaki wanamshangaa iweje yupo nje wakati huu.



    Hakuna aliyemhoji. Aliwahadaa ili aweze kupoteza muda ili magari mengine yaweze kufika mbali na sehemu walipo. Hakuna aliyekuwa na wasiwasi naye kwani walijua ni mwenzao.



    Ghafla Antony alitoa bastola yake aliyokuwa ameifunga kiwambo cha kuzuia sauti na kuwafyatulia wote. Aliwapeleka hadi walipo kina John na Max na kuwaweka katika chumba kimoja na kuwatoa nguo zao ambazo John na Max walivaa na kuchukua pia silaha zao.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Aminata aliachwa nao kwenye kile chumba ambacho kilikuwa nje ya ile hoteli bila ya mtu yeyote kuingia. Aliwataarifu wahusika wa hoteli ile na kuwatolea kitambulisho na kuwaeleza kwamba wako kazini na hivyo wasiogope wala kushiriki kwani ni hatari.



    Kuona vile watu waliokuwa kwenye ile hoteli waliamini na kuwapa nafasi ya kufanya wanalolitaka bila kutoa taarifa kama Aminata alivyowaagiza wakae kimya wasubiri kitakachotokea.





    *****

    Antony, Max pamoja na John walitoka na kuelekea kule yale magari yalikoelekea wakipitumia lile gari alilolisimamisha Antony. Walifika na kufunguliwa mlango mkubwa na walipita bila ya kuwa na wasiwasi wowote. Baada ya kufika eneo la kupaki magari walishuka na John na Max wakaanza kumfuata Antony.



    Wakiwa wamebeba mabegi yao na silaha kama baadhi ya askari walivyokuwa wamebeba. Waliwasiliana na kuanza kuyatega mabomu kila upande kuhakikisha wanaliporomosha jengo zima.

    Helkopta iliyokuwa imewapeleka Mosses na Steve ilikuwa ikirudi na hivyo askari wote walitakiwa kusimama katika paredi tayari kwa kuwapokea na kusikiliza machache kutoka kwao kama ratiba ya siku hiyo ilivyokuwa ikisema. Kwa John, Antony na Max hilo ililikuwa kazi kubwa sana kwao na hivyo waliamua kukimbia na kwenda kujificha.



    Baada ya Mosses na Steve kuingia na kuona vikosi vyote vikiwa vinawasubiri. Mosses aliwapa taarifa juu ya vifo vya askari ambao alikuwa amewatuma kwenda kuwaangamiza kina John. Kinyume na matarajio yake. Walishindwa kufanya hivyo na hivyo wote waliuliwa.



    “Tumepoteza wazembe…wazembe ambao nimewapa kazi ya kuwashika watu wawili tu lakini watu hao wawili wamewashinda na kuwaua kabisa….inaonekana ni kiasi gani mlivyo wazembe,” Mosses aliongea kwa kufoka. Hakuamini kama askari aliowatuma wameuliwa. Hasira zilimpanda sana.



    Kina John walisikia yaliyosemwa na Mosses. Waliamua kutoroka ili wakishatoka wayaache mabomu yalipuke yenyewe. Walitaka kutafuta njia ili watoke kwani isingekuwa rahisi wao kutoka kwani wangeonwa kwa kuwa askari wote walikuwa wameitwa sehemu moja.



    Wakati akiendelea kutoa maneno makali kwa askari wake. Ghafla alisikia sauti ya risasi iliyofyetuliwa na Max kumlenga mmoja wa askari aliyekuwa mlangoni ambaye aliwaona. Hali hiyo iliwashtua na hivyo Steve aliwaamrisha askari kadhaa waende wakaangalie ni nini. Kufika tu, walikutana na kichapo kikali. John na Max waliwamiminia risasi huku Antony akisonga mbele kueleke mlangoni. Ghafla walishangaa askari wengi wakija na kuanza kuwarushia risasi huku wakikimbia. Mosses alijua mambo yameshaharibika.



    “Tusitoke hadi tuhakikishe wanaisha…. Sio wengi sana hawa. Wavuteni kwenye maeneo tuliyotega mabomu. Ila tuweni waangalifu maana baada ya dakika ishirini na tano sasa yatalipuka. Itabidi tuwahi kutoka nje.



    Risasi zilianza kurindima. Walifanikiwa kuwaua baadhi yao huku wengine wakijaribu kukimbia. Waliwafuata huko huko walikokwenda.



    Mosses na Steve walionekana kuchanganyikiwa baada ya kuona mashambulizi ya ghafla yaliyozuka katika jumba lile. Alipiga simu na kuwaarifu vikosi ambavyo vilikuwa mgodini vije visaidie mapambano.



    “Nani kawaruhusu hawa wajinga kuingia?” alifoka sana Steve huku akiitoa bastola yake na kuikoki vizuri.



    Aliona kama Mosses ndo aliyesababisha yote yale kwani kabla ya kuwa naye hakuna baya lililomtokea. Na sasa vikosi vyake na mipango yake inaharibika. Mosses na yeye alijua kwamba Steve lazima atamgeuka na hivyo aliamua kutoka kwa lengo la kukimbia.

    Antony na Max walikuwa wameshaingia na kuanza kushambulia katika chumba alichokuwa Steve na baadhi ya askari.



    Waliwaua wote na kubaki na Steve ambaye hakuwa na ujanja wowote wa kutoroka zaidi ya kusalimu amri na kuweka silaha chini. Baada ya kuona askari wengine wakija Antony na Max walianza kuwashambulia pamoja na kumpiga risasi Steve na kumuua palepale huku wakiwashambulia askari waliokuwa wakiongezeka mmoja mmoja.



    Antony alipigwa risasi ya begani na hivyo alikuwa akitumia mkono wa kushoto huku akimhimiza Max watoke nje. Max alikuwa amemshikilia na mkono mmoja huku akiendelea kuwashambulia hadi walipotoka nje huku akizidi kuwashambulia.



    *****

    Aminata na Francis walikuwa njiani wakiwafuata kina John. Huko alikutana na kundi la askari wa Mosses wakielekea kwenye jumba la Steve kusaidia. Waliwashambulia kwa risasi mfululizo hadi kuhakikisha wameisha wote ambao nao walikuwa wakijibu mashambulizi kwao.



    Walifika muda mfupi baada ya kusikia mashambulizi yakiwa makali. Aminata na Francis walifika mbele ya lango kubwa na kuwashambulia askari waliokuwa wakiwasubiri kina John.



    Alimwona Mosses akiifuata helikopta kwa lengo la kutoroka lakini mara helikopta ile iliondoka na hivyo hakuweza tena kuipata. Aminata aliwahi na kuilenga ile helikopta na kuilipua.



    Mosses alishtuka baada ya kuona imemuacha na kisha kulipuka. Alikuwa bado hajamwona Aminata.



    Ghafla alimwona Aminata akimfuata. Alianza kumrushia Aminata risasi ambazo zilikuwa zikimkosa huku Aminata akizidi kumsogelea. Alimfyatulia risasi ambayo ilimpata begani na kukaa chini. Mosses alikuwa akiangaliana na Aminata pasipo kuamini kwamba hajaambulia chochote kutokana na mipango yake.



    Hasira zilimvaa huku akihema sana. Bastola yake ilikuwa mbali na alipo na hivyo hakuweza kuiokota. Alisimama ghafla na kunza kukimbia. Alifanikiwa kumtoroka Aminata lakini mbele yake alikuwa amesimama John ambaye alikuwa ameshamwona.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Aminata ambaye alikuwa akija kasi kumfukuza Mosses alishangaa kumwona Mosses akiwa amesimama ghafla huku akiwa ameshika bega. Mbele alimwona John. Alikuwa amemnyooshea bunduki Mosses tayari kwa kuifyetua kumlenga.



    Mosses alishindwa la kufanya na kujikuta akiwa amezungukwa na John na Aminata. Mirindimo ya risasi iliendelea huku Mosses akionekana kukata tamaa.



    “Ulijua hatutakukamata…. Mshenzi mkubwa wewe.. ulitaka kututisha na jeshi lako la mamia ya wanajeshi… Uwezo wa kikosi chako haukuuweza sasa umeungana na Steve… tumegundua kwamba ulifanya hila za kuchukua mgodi wa mzee wetu Amigolas kwa kutumia Hati Feki lakini tuliurudisha katika himaya yetu….

    Ulimuua mwenyewe na sasa tumekupata… huwezi kutusumbua mtu kama wewe…. Tuligundua mengi kuhusu wewe, sasa mwisho wako umefika…. Hata kama ulifanikiwa kutoroka huwezi kukimbilia kokote… huwezi kutukimbia sisi… Tulijua tu ipo siku tutakukamata… na sasa hatukupeleki mahala popote kwani sasa wewe ni halali yetu… utakuwa maiti kama ulivyofanya kwa ndugu zangu,” John alikuwa anaongea kwa hasira na uchungu huku akiangaliwa na Aminata. Mosses alikuwa akijivuta kuelekea sehemu ambayo bastola yake ilikuwepo. Ghafla John alifyetua risasi ambayo ilimpata ya kichwa Mosses ambaye alikuwa akitaka kumfyetulia risasi John baada ya kuishika bastola yake. Alianguka chini na kufariki pale pale.



    “Aminata,” aliita John huku akimfuata baada ya kuangalia saa yake na kugundua kwamba ni dakika mbili tu zilibakia kabla ya mabomu kulipuka na hivyo.



    “John,” aliitikia Aminata huku akimfuata John. Walianza kukimbia wakielekea katika lango kuu la kutokea. Walikuwa wakisikia milio ya risasi huku wakiwaona Antony na Max wakirudi nyuma huku wakikimbia kuwafuata wao.



    Mabomu yalianza kulipuka wote wakiwa wameshatoka nje ya lango kuu. Walisimama karibu na gari ambalo alikuja nalo Aminata na kuangalia lile jumba lilivyokuwa likilipuka.



    “Antony… una nini,” Aminata alimuuliza Antony ambaye alikuwa ameshikilia bega lake la kulia huku likivuja damu.



    “Tuwahini tumpeleke hospitali alipigwa risasi na wale washenzi.. tuwahini,” alisema Max huku wote wakiingia ndani ya gari ili kuwahi hospitali. Ghafla magari ya polisi yalikuwa yamefika na kuwasimamisha bila ya kujua wao ni nani. Wa kwanza kutoka alikuwa ni Max ambaye alitoa kitambulisho na kuwaonyesha.



    “Mkimaliza kutukamata sisi hakikisheni na huyo waziri wa ulinzi anatiwa nguvuni… anayo kesi ya kujibu,” alisema John huku akitoka nje ya gari na kusimama na Max. polisi walielekea katika jengo lile lililokuwa likiwaka moto baada ya kulipuliwa na kuanza kukagua.



    Watu walikuwa wengi waliokuja kushuhudia baada ya kusikia mlipuko ule. Wengi walikuwa wakishangilia kutokana na manyanyaso waliokuwa wakipewa na askari waliokuwa wakilinda jumba lile huku wengine wengi wakiuliwa pale walipojaribu kuingia katika barabara iliyokua mefichwa kuingia katika jumba lile.



    “Wazari wa Ulinzi anahusika…. Haiwezekani askari wote wale wamilikiwe na mtu mmoja alafu ni mfanyabiashara,” alisema Max wakiwa nje ya Hospitali ya Mount Meru wakisubiri matibabu ya Antony.



    “Tusimamieni tuhakikishe anashtakiwa.”





    *****

    Ilikuwa ni Jumapili wiki moja baada ya shambulio lile. Wengi walikuwa wakilifuatilia kwa karibu ili kujua hatima ya waziri wa ulinzi ambaye inasemekana alihusika pamoja na kundi lililokuwa likiongozwa na Steve na Mosses Ndula.



    Katika taarifa ambayo ilikuwa ikirushwa hewani, baadhi ya mambo yalikuwa yakizungumzia ambayo yaligusa sana hisia za watu na kufnya kila mtu afatilie kwa makini sakata hilo.



    “Habari ambazo zimetawala katika mkoa wa Arusha na nchi nzima zinasema kwamba, Waziri wa Ulinzi alishirikiana na mfanyabiashara maarufu kuanzisha kambi ya siri ya kihalifu iliyokuwa inatishia amani katika mkoa wa Arusha nan chi nzima. Inasemekana ya kwamba waziri huyo alichukua baadhi ya wanajeshi wan chi na kuwapeleka ili kuimarisha kambi hiyo ya kihalifu iliyokuwa ikisimamiwa na mfanyabiashaara mkubwa Steve Muro. Kambi hiyo ilikuwa Mererani karibu na migodi ya madini ambayo ni maarufu ya Tanzanite na ilikuwa ni kambi ya siri ambayo haikuwa rahisi kujulikana.



    Tuhuma zinapelekwa kwa waziri huyo ambaye ameshindwa kusimamia usalama wa nchi kwa kufanya mambo kwa masilahi yake binfsi. Pia katika kambi hiyo alikuwapo mkuu wa vikosi hivyo ambaye alijulikana kwa jina la Mosses Ndula ambaye awali inasemekana kuwa ndiye aliyekuwa akifanya biashara za magendo na baadhi ya viongozi wakubwa wa nchi pamoja na uhalifu.



    Katika tukio ambalo linathibitishwa kwamba alihusika nalo ni lile la mauaji ya mzee Amigolas mfanyabiashara mkubwa wa madini ambaye alikuwa ni mpinzani mkubwa wa Steve Muro pamoja na familia yake kisha kuiba hati ambayo hata hivyo ilisemekana kuwa ni feki na hivyo baada ya watoto wake mzee Amigolas, John na Antony kubaini hayo, waliamua kufanya kila wawezalo ili warudishe haki zote chini yao ambapo walifanikiwa.



    Kwa sasa polisi wanamshikilia waziri huyo ili aweze kufikishwa katika vyombo vya sharia ili kujibu tuhuma hizo.”



    “Mmesikia,” Max alisema akiwaambia John na Aminata wakati wakielekea nyumbani kwa Antony kumjulia hali. Antony alikuwa akiishi peke yake katika nyumba ambayo aliinunua katika maeneo ya Sombetini. Aliwaacha John pamoja na mke wake Aminata wakae katika nyumba yao iliyokuwa maeneo ya Njiro.



    “Niliipeleka ile ripoti kwa maofisa wa polisi ili iweze kusomwa kwa wananchi wajue ukweli wa mambo. Nchi ilikuwa imeshaanza kugeuzwa mradi wa wachache. Tumefanikiwa kumdhibiti.

    Antony alirudi akitokea Mererani ambako alienda kusimamia na kuhakikisha hali katika mgodi wao unakuwa salama. Aliwakuta kina John na Aminata wkiwa nje ya nyumba yao pamoja na mtoto wao Amigolas na Max.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Mambo yatakuwa mazuri, kwa muda huu mchache nimeshamalizana na wote.”



    “Subiri kwanza,” alidakia John…. “Francis umempa kazi,” aliuliza John.



    “Eeeh, kweli. Nakumbuka ulimwahidi.”



    “Ndio, yupo kazini na kazi zimeanza,” Alisema Antony huku akikaa chini kwenye bustani ya majani karibu na Amigolas.



    “Poa, nadhani mambo hata huku si mabaya,” alisema John. Wote walionekana ni wenye kujivunia jambo moja tu…. USHINDI.





    MWISHO



0 comments:

Post a Comment

Blog