Search This Blog

Sunday 22 May 2022

SHUJAA WA TAIFA - 1

 







    IMEANDIKWA NA : HANS MASLEEN



    *********************************************************************************



    Simulizi : Shujaa Wa Taifa

    Sehemu Ya Kwanza (1)

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wananchi katika nchi tulivu iliyosadikika kuwa na Amani, utulivu pamoja na demokrasia ya hali ya juu mara taswira hiyo inaondoka ghafla katika vichwa vya watu, na yule mkubwa wa nchi waliomwamini na kumkabidhi nchi wakiamini ile hali ya awali iliyokuwa ikifanywa na viongozi waliopita basi angeweza kuiondoa, hakika walijidanganya kwani ilikuwa ni tofauti.

    Wengi waliamini kuingia ndani ya ikulu ya nchi hiyo rais huyo aliyewahi kuziteka nyoyo za wananchi wake kwa hali ya juu hasa katika kipindi chake cha kampeni kwa ahadi zake tamu na zilizokuwa zikililiwa na wananchi kwa muda mrefu, ghafla hali ikabadilika na kutokuwa kama ilivyotegemewa baada ya kupita kipindi chake cha awali cha uongozi wake wa katika miaka saba.

    Wananchi walibaki kimya na kila aliyeamua kuhoji kitu tena kwa lengo la kuirekebisha serikali hiyo aliishia kupotea kimya kimya kwa wananchi hao.

    Hali ikawa si shwari tena katika nchi hiyo, kila kitu ndani ya nchi hiyo kilibaki mikononi mwa serikali. Si vyombo vya habari, taasisi za kifedha na hata kampuni za watu binafsi zilirudisha usajili na kuwa katika himaya ya serikali hali ambayo ni tofauti na hapo awali.

    Wananchi n ahata wanasiasa wa upinzani wakabaki kimya wakiisikiliza nini serikali inahitaji ndio ifate. Hali ikawa tafrani kabisa na kila mtu alitamani ahame katika nchi hiyo ila ilishindikana kwa kile kinachodaiwa kuficha usiri wa mambo yote yanayotokea ndani ya nchi yasitoke nje, ikafikia hatua hata ukihitaji kwenda nje ya nchi unakaguliwa kwanza kama una habari yeyote kulihusu taifa hilo. Na kibaya Zaidi kinakuja pale unapokutwa na habari za taifa basi jela ndo huwa fikio lako la mwisho kabla ya kufa.

    Vyombo vya habari vya nchi hiyo vilivyo chini ya serikali bado viliendelea kuficha usiri wa yote yanayotokea ndani ya taifa hilo, na mitandao ya kijamii yote ikazimwa, basi nchi ikabaki kwenye giza lililonakshiwa kwa uongo wa vyombo vya habari.



    KUSIKILIZA SEHEMU YA KWANZA YOUTUBE IKIWA IMESIMULIWA KWA UMAHILIVWA HALIVYA JUU BOFYA LINK HII>> https://youtu.be/Dr_Skzkbero AU YOUTUBE SEARCH SHUJAA WA TAIFA 01



    SHUJAA WA TAIFA

    SEHEMU YA KWANZA

    Katika jumba tukufu ndani ya nchi ya zambe si jumba lingine bali mahali ipatikanapo ofisi na makazi ya raisi wa nchi hiyo MH.DK. Elias Stamphord yaani ikulu,vijana watatu waliovalia suti nyeusi huku wakinogeshwa na miwani meusi iliyopendezesha nyuso zao wanaonekana wakipiga hatua mara baada ya kushuka ndani ya gari.

    Wanatembea staili ya mmoja kuwa mbele kwa hatua chache na wengine wawili kumfuata kwa nyuma, mmoja akiwa upande wake wa kushoto na mwingine akiwa upande wa kulia.

    wanalifikia geti la kuingilia ndani tofauti na la kwanza waliloliacha mara baada ya kuingia na gari lao.

    Saluti inatolewa kwa kijana huyo aliye mbele, ni wazi anaonekana kuwa na wadhifa mkubwa ndani ya jengo hilo. Na kwakuwa taarifa za ujio wake zilishatolewa kwa walinzi wote wa ndani humo hivyo alipita bila wasi akiwa na vijana wenzake hao wawili wakimfuata kwa nyuma.

    Baada ya kona za hapa na pale wakafanikiwa kuingia katika chumba maalum cha wageni ndani ya jumba hilo tukufu.

    Wanakaribishwa kwa bashasha na wasaidizi wa rais na kuketi katika viti vya thamani ndani ya chumba hicho.

    Muda si mrefu rais bwana ELIAS STAMPHORD anawasiri akiwa mwenye bashasha.

    Anawapa mikono wakiwa wamesimama ikiwa ni ishara ya salamu kwa kumuanza kijana yule aliyeonekana kuwa ndiye kiongozi wa vijana wenzake wawili,kisha wanafuatia wale wengine. Wanaketi chini baada ya salamu hiyo.

    “naam kijana wangu, habari za wizara yako zinasemaje huko!” rais alianzisha mazungumzo, ni wazi kabisa kijana yule alikuwa ni waziri, je ni waziri wa nini? Na amefuata nini kwa rais ? ebu tuendelee kufuatilia kisa hiki hatua kwa hatua , neno kwa neno ili kuweza kuburudika sambamba na kuelimika.

    “aaah wizara yangu nashukuru ipo njema sana, japo changamoto ni nyingi kama ujuavyo wizara hii ya mambo ya ndani ina maadui wengi sana sanjali na kuimarisha ulinzi wa nchi lakini anyway tuongelee lililonileta” kijana huyo ambaye kutokana na kauli zake tunapata kufahamu kuwa ni waziri wa mambo ya ndani, aliongea na kunyamaza kidogo.

    Rais akabaki kumsikiliza kwa umakini.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “mkuu pamoja na mipango yote nayokusukia kuhusu nchi hii naona bado sijaridhika vile navyohitaji, nahitaji kuiongoza kabisa hii nchi” kijana huyo ambaye ki umri alisomeka kati ya miaka 30 hadi 32 hivi aliongea kauli iliyomfanya rais mwenye umri wa miaka 54 apaaliwe na mate kisha kukohoa kabisa.

    “ati sijakuelewa una maanisha nini labda?” rais akahoji baada ya kuacha kukohoa.

    “ha ha haaaaa, haujui nachomaanish” waziri huyo akanyanyuka na kumsogelea rais kisha kumchezea chezea ndevu. Ni wapi aliupata ujasiri huo waziri huyo wa kudiriki kunyanyua mkono wake na kuchezea kidevu cha bosi wake? Si bosi wake tu bali ni bosi wa wanazambe wote? Hakika ilikuwa ni dharau Dhahiri.

    “utaelewa muda si mrefu nachoenda kukufanyia” akaongea waziri huyo huku akimwinamia rais huyo huku mguu wake wenye kiatu akiwa kauweka katika paja la mkuu huyo wa nchi ambaye alikuwa akiogopeka na watumishi wote wa serikali yake.

    “paaaaaaaaaaaaaaaaaaa!!’ ni sauti ya kibao kichotua katika shavu la waziri mara baada ya rais kuchukizwa na dharau ile aliyokuwa akifanyiwa mbele ya watumishi wake na walinzi pia.

    Waziri alichukizwa na kibao kile alibaki ameshikilia shavu lake kwa uchungu mara baada ya kujirudisha nyuma kutoka kwa rais.

    Waziri akabaki anamtumbulia macho rais kwa hasira za hali ya juu. Akamsogelea na kurejeshea kofi lile tena lililo zito haswa Zaidi ya alilopewa yeye.

    Rais alijiinamia kuugulia kofi lile lakini alipojinyanyua alishangazwa na walinzi wake kuwaona wamesimama tu pasipo na majibu yeyote. Alishangaa sana.

    “mkamateni huyo!” akatoa amri lakini wapi hakuna aliyetii amri hiyo.

    Akawageukiwa walinzi wake huku akiwa mwenye uso uliojaa sintofahamu ya hali ya juu, “mmeanza kushindwa kazi ee?” akawahoji kwa ghazabu

    “mhe.dkt. Stamford, unajisumbua bure hakuna yeyote atakayejibu ama kutii amri zako, am the man of the match now… ulikosea sana uliponikabidhi wizara hii nyeti, na sikufanya makossa pale uliponifanya kuwa mshauri wako nilitumia chansi hiyo vizuri kwa kukuambia uombe walinzi wako wa ikulu wawe walinzi kutoka nchi ya mbali, hukujua tena mpango wangu pale nilipokupangia mkuu wa majeshi ya usalama kwani watu wote uliowaeka hapo walikuwa wanajua kabisa mipango yangu hivyo nasikitika kukuambia kuanzia sasa nchi hii itaenda vile navyotaka mimi lakini kwa kivuli chako” waziri aliongea maneno yaliyomchanganya rais, ni wazi yalikuwa na ukweli ndani yake kwani kitendo cha rais kupigwa ndani ya ikulu tena mbele ya walinzi wake kilithibitisha hilo.

    “sasa kama unahitaji uhai wako ubaki katika dunia hii, naomba tufanye kazi kwa kushirikiana ambapo chochote kinachotakiwa kufanywa na rais utafanya wewe as long as wananchi wanakufahamu kuwa wewe ndiye rais wao na wengine wasioufahamu ukweli huu unaoufahamu wewe leo hii”akaongea maneno hayo waziri huyo huku akimeza mate na kuendelea,”kwahiyo wewe utafanya kazi kwa amri yangu na si kama hapo awali ambapo wewe ndiye ulikuwa mkuu wangu, sasa mkuu ni mimi,lakini mbele za wananchi ntabaki kuwa mdogo kwako na kukusifia, vinginevyo hautoweza kuiona tena nchi yako tena sio kwa kukuua kirahisi, utapata mateso maalum hadi pale mungu atakapopenda,sawa?”

    Maneno hayo mazito na yasiyotegemewa kutoka katika kinywa cha kijana huyo aliyeaminiwa kwa asilimia zote na rais wake, yakamuacha hoi rais na mara presha ikampanda.

    Haraka alikimbizwa katika chumba cha matibabu ndani ya ikulu hiyo tayari kwa kupata matibabu.





    *******

    D’Oen ni kijana aliyefanikiwa kuhitimu vyema mafunzo yake ya kijeshi katika nchi ya zambe. Awali D’oen alikuwa akitamani mno nafasi hiyo japokuwa alitoka katika familia ya Maisha ya kimasikini lakini haikumuingia ugumu sana kupata kazi hiyo mara baada ya kutuma maombi yake.

    Hakufanikiwa kusoma sana lakini alikuwa na ujuzi wa kipekee wa kurenga shabaha, na hata mara kibao kijijini kwao kulipokuwa kukitokea mashindano ya shabaha katika sherehe za siku muhimu ya taifa alikuwa akiibuka kidedea. Kutokana na sifa hiyo aliweza kupitishwa jeshini kwa wepesi mno, na kigezo chake cha urefu wa futi saba kilimpa credit kubwa kuingia ndani ya jeshi hilo katika nchi yao.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Anakabidhiwa kitengo cha utunguaji almaarufu kama sniper katika jeshi hilo, na hata mara kibao katika mashindano ya kijeshi ya kimataifa ya utunguaji alikuwa akishika nafasi ya kwanza, hivyo aliweza kulipa heshima kubwa mno jeshi hilo.

    Wikiendi moja akiwa na Rafiki yake kipenzi aliyetambulika kwa jina la hance ambao wote ni maaskari lakini wakiwa katika mavazi ya kiraia waliingia mtaani muda wa usiku. Ndani ya bar maarufu iendayo kwa jina la kismart katika jiji la ntovo, jiji ambalo ndiyo makao makuu ya nchi hiyo ya zambe,bar ambayo inasifika kuuza wadada na wakaka, D’oen akiwa na hance waliamua kuitumia bar hiyo usiku huo.





    “hey mrembo” hance mkaka ambaye wanawake kwake walikuwa kama dhahabu maana hakuacha kutupia macho au swaga pindi mmoja ampitiapo karibu, akaongea akimwita kwa kumpiga makalioni mdada aliyekuwa akikatiza karibu yake.

    Mdada huyo akageuka huku akijichekesha, ni wazi alikuwa ni muhudumu ndani ya bar hiyo.

    Hance akamvuta kwa mkono wake kuushikisha katika kiuno cha mwanadada huyo, akambania mwilini mwake huku akimpatia mabusu motomoto.

    “kama kawaida tuletee kile kinywaji chetu kile bariiiiidi alafu na wewe uje pamoja na warembo wenzako” hance akaongea huku akimramba ramba dada huyo sehemu mbalimbali za mwili wake.

    Kipindi chote hicho D’oen alibaki akitabasamu tu kumuangalia mwenzie aliye mtundu katika kuwafanyia mambo ya ajabu wadada wa bar hiyo mara zote afikapo.

    Mrembo huyo akajichomoa katika mikono ya hance mara baada ya kuona kuchezewa maungo yake kupitia mikono ya kijana huyo kumezidi.

    Akaondoka huku akijichekesha bado akiwa anamwangalia hance kwa tamaa ya kumlia pesa zake.

    “aka katoto nakakubari sana, aaah kana kijungu bwana” asante akaongea akimwangalia D’oen

    “kazuri ila mie matwipwa twipwa vile aaah sio ugonjwa wangu kabisa” D’oen nae akachangia mada hiyo.

    “aaaah kaka wale ndo watamu!” hance akaongea huku akimchapa chapa D’oen kifuani kama ishara ya kunogesha mazungumzo.

    “mimi waaapi, ngoja kizarish changu kije”

    “lazima aje nacho ila ni chombo nacho kizarish”

    Wakiwa wanaendelea na mazungumzo mara mrembo yule waliomuagiza alete vinywaji akaonekana akizipiga hatua kuelekea katika meza ya maaskari hao akiwa na chupa za vinywaji huku akiwa na msichana mwingine pembeni yake ambaye ni mwembamba, mrefu na mweupe si haba!

    D’oen na hance wakageuza macho yao kuwatazama. Macho yaliwatoka pima.



    Alikuwa ni mwanadada Zarish, mwanadada aliyejipatia umaarufu mno katika jiji la ntovo hasa hasa katika bar hiyo ya kismart kutokana na uwezo wake wa kucheza staili mbalimbali za mziki ndani ya bar hiyo.

    “hello!” Zarish akatoa mkono kumpatia D’oen baada ya kumfikia.

    “hello Zarish, mzima wewe!” D’oen akaongea huku akimzungusha Zarish kwa kupitia mkono aliomshika na kumfanya amgeuzie sehemu za nyuma zilizo za wastani lakini zilinoga kutazamwa.

    Kisha akamkalisha kwenye mapaja yake na kuanza kuzungumza nae kimahaba. Wakati huo nae afande hance alikuwa amemkalisha mrembo wake kwa staili ile ile kama aliyokalishwa Zarish. Stori ziliendelea na huku vinywaji vikiendelea kugigidwa.

    Mara D’oen anamnyanyua Zarish na kumwambia kuwa anaelekea maliwatoni mara moja, hivyo anampiga mabusu na kuelekea upande wa maliwatoni.

    Hatua chache kabla ya kuzama katika vyoo , akiwa katika kordo ya vyoo hivyo mara aliisikia sauti kutoka katika moja ya choo hicho.

    “…..eee hakikisheni mnaandaa kabisa silaha,kabla hawajafunga tuwe tushamaliza kazi..”

    D’oen akajibanza kuweza kusikiliza maneno hayo yanahusu nini.

    “na kule bank msijali ntaongea na ntawapanga askari vizuri kesho tunavamia sawa?” sauti ya kijana huyo ikasikika ambayo ni wazi ilikuwa ni maongezi kupitia simu.

    Baada ya muda kidogo kijana huyo akatoa tena mazungumzo ni wazi ilikuwa ni simu nyingine mara baada ya ile ya kwanza kukatwa.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “…naitwa G master, kesho saa saba mchana nakuja kuvamia katika bank yenu, ntakuwa na silaha kali sana za kivita kwahiyo jihandaeni”

    Akakata simu mara baada ya kauli hiyo kisha akaitoa laini hiyo kwenye simu yake na kuitupa kwenye sink la choo.

    Akaanza kupiga hatua kutoka ndani ya chumba hicho. D’oen aliposikia mlio wa viatu vya kijana huyo akakimbia haraka kujificha ili asionwe na mtu huyo lakini lengo la kumgundua mtu huyo aliyekuwa akiongea kupitia simu ni nani bado lilibaki akilini mwake.

    Akatafuta sehemu nzuri ambayo alihakikisha anaweza kumuona.

    Kijana huyo aliyetambulika kwa jina la G master akapita alipojibanza D’oen, pasipo kumuona D’oen akaondoka eneo hilo. D’oen aliweza kuigundua sura ya mtu huyo lakini hakuwa akimfahamu.

    Akapuuzia na kuendelea na biashara yake iliyomleta mahali hapo.

    Alijisaidia na alipomaliza alirejea kwenye meza yake lakini alishtuka baada ya kumuona kijana yule aliyemsikia chooni akiongea na simu akiwa katika moja ya meza jirani kabisa na ilipo meza yao. Ni kweli walionekana walikuja kikazi Zaidi maana alikuwa na vijana wengine wanne waliojazia miili yao haswaa.

    “oya mic hapa si mahali salama tena” D’oen akamnongoneza hance sikioni ambaye muda huo alikuwa katika dimbwi zito la mahaba ya kushikana shikana na mrembo wake. Mic ni jina waitanalo maaskari wanaofanya kozi moja.

    “kuna nini tena aaaaaah” hance aliuliza kilevi

    “unawaona wale?” D’oen akaendelea kuongea kwa kumnong’oneza kumuoneshea vijana wale.

    Hance akageuka kiulevi ni wazi kabisa pombe ilishamkolea kichwani mwake.

    “wachumba tu wale” hance alijibu huku akiwaangalia pasipo na kujua alichokusudiwa kuoneshewa watu hao.

    “wale hawapo kiusalama na mahali hapa tena si salama, wana silaha kali sana tuondoke Rafiki yangu”

    “ooo nani kakwambia, acha bwana mambo yako hii ni sehemu ya starehe sio sehemu za kivita usilete uafande wako hapa” hance aliongea kwa sauti ya juu ya kilevi.

    Sauti hiyo ilipenya moja kwa moja hadi masikioni mwa G master na neno uafande liliingia vilivyo masikioni mwake, akawatazama D’oen na hance kwa makini kabla ya kuinuka alipoketi na kujisogeza katika meza yao.

    “hamjambo wachumba!” akaongea huku akimchezea nywele Zarish na baadae kumwachia busu la mdomo lililomkera sana Zarish na kumsukuma.

    “broo mbona sio ustaarabu huo?” D’oen akaongea akimsukuma G master

    Ni kama alikuwa amemwaga mafuta ya petrol juu ya njiti ndogo ya kiberiti iliyo na moto. G master alionesha hasira za waziwazi

    “nani aliyekupa ruhusa ya kuugusa mwili huu?” G master akaongea kijazba

    Kabla D’oen hajajibu lolote alishtukia ngumi nzito ikitua upande wa kushoto wa sikio lake,Kabla hajatulia G master akaichukua chupa tupu ya kinywaji iliyo mezani na kuivunja kisha kumfuata nayo D’oen kwa ajili ya kuizamisha katika mwili wake.



    hance alipomuona g master akielekea upande wa Rafiki yake ndipo alinyanyua moja ya kiti cha plastiki kilichopo pembbeni yake na kumtandika nacho G master mgongoni, hali iliyomfanya aghailishe kumfata D’oen na kumgeukia hance huku akiwa amezira kwa jazba.

    Hance akaanza kurusha chupa tupu za bia kumtafutia G master. Hapo ndipo kizaazaa kilianza ndani ya bar hiyo mara baada ya watu kujikimbiza huku na kule kwa lengo la kunusuru roho zao. D’oen alichokifanya wakati huo si tena kupambana na mtu huyo badala yake alimkimbilia Rafiki yake baada ya kumpita g master aliyesimama kumuangalia hance kwa hasira, akamshika mkono kisha kutokomea nae kwenye kundi la watu walioingiwa na taharuki.

    “pumbaaaavu piga risasi juu” G master alikoroma baada ya kuona D na hance wakitokomea.

    Milio ya risasi ikaanza kurindima ndani ya bar hiyo.

    Lakini hance na D’oen wao walifanikiwa kutoka ndani ya bar hiyo na kuishia zao.

    Mule ndani hapakuwa tena sehemu salama kwani G master alikuwa na hasira si haba, aliamuru watu wake wavunje na kuharibu mali ndani ya bar hiyo huku wakifanikiwa kutoweka na mapato ya bar ya siku hiyo.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Watu wengi waliumia na wengine kufariki kupitia taharuki hiyo, lakini cha kushangazwa serikali haikuruhusu habari hiyo itangazwe.

    Hance na D’oen wakiwa moja wa wahanga wa purukushani zile walishangaa sana taarifa ile sensitive kutoweza kutangazwa katika vyombo vyao vya habari siku iliyofuata. Ikabaki sintofahamu kubwa ndani ya kichwa cha kijana shupavu mpenda haki kwa kila mtu,D’oen!

    Na hata baadae alipozisikia taarifa juu juu kutoka kwa moja ya maafande wenzake kuwa moja ya tawi la benki katika jiji hilo kuvamiwa na majambazi na kuchukuliwa pesa nyingi mno,aliumia mno. taarifa hiyo pia ilimpa mshtuko baada ya kupitia magaazeti yote na kusikiliza vyombo vya habari lakini bila mafanikio ya kuiona taarifa hiyo.

    Aliifikiria sauti ya kijana G master ikitokea moja ya chooni katika bar ya kismet ikiongelea swala lile la kuvamia benki “…naitwa G master, kesho saa saba mchana nakuja kuvamia katika bank yenu, ntakuwa na silaha kali sana za kivita kwahiyo jiandaeni”

    ,hapo ndipo aliamini kuna mtu mkubwa anahusika nyuma ya kivuli cha G master na kundi lake.

    “haiwezekani kuna mtu mkubwa atakuwa anahusika, iweje mtu apige simu kabisa kutoa taarifa na kweli wanaiba tena bila kukamatwa? Kuna mchezo unachezwa na mtu mkubwa hapa” alijisemea huku akiwa mwenye uchungu moyoni kuliko uchungu wenyewe.

    D’oen aliumia sana kutoweza kufanya lolote kuisaidia nchi yake katika shetani lile la madaraka tena ya kulevya,kuna muda alitamani sana kuresign(kujihudhuru) kutoka katika jeshi hilo mara baada ya kuona thamni yake kama kiongozi wa usalama wan chi haipo.

    Hapo kipindi alipokuwa raia wa kawaida alikuwa akifikiri kati ya watu waliokuwa wakiheshimika na serikali katika nchi hiyo basi wanajeshi hawakukosekana lakini hali ilikuwa tofauti baada ya kuingia katika jeshi hilo.

    Alishuhudia wakubwa wachache katika jeshi hilo waliokuwa karibu na uongozi wa serikali kuu ndio pekee wakilifaidi jeshi hilo, wanajeshi wote wa levo ya chini walibaki kutothaminiwa japokuwa mchango wao ulikuwa mkubwa mno katika jeshi. Hawakuweza kufanya lolote kukabiliana na hali hiyo kwani kwa taratibu za jeshi ilikuwa ni lazima amri ya mkuu ifatishwe,

    Na alichofanikiwa katika kulikontrol jeshi hilo bwana Elias Stamphord ambaye ni rais wa nchi hiyo ni kile kitendo cha kumkabidhi jeshi hilo kibaraka wao ndugu.jenerali HOMBABE. Hakika walifanikiwa mno kwani Amani iliendelea kutawala japokuwa kiuhalisia hakukuwa na Amani hata ya macho bali ni woga na uvumilivu tu kutoka katika jeshi hilo.

    Sauti mbali mbali za kupinga uonevu zilipazwa lakini hazikuishia kokote, bwana Alberto Banguli ambaye ndiye alikuwa waziri wa mambo ya ndani wa nchi hiyo ambapo na nyuma ya pazia ndiye aliyekuwa rais wan chi hiyo kwa siri, alifanikiwa kuzizima sauti hiyo kwa kutafuta mizizi yaani viongozi wa sauti hizo.

    Taratibu walikuwa wakitekwa kimya kimya pasipo yeyote kujua na kupotezwa kabisa. Taifa liliingiwa na hofu na kama mshumaa wananchi wakabaki wakiangalia tu na kuugumia moyoni bila kusema lolote.



    ******



    Mwanadada Ashey-tiffa ama tiffa kama wengi walivyozoea kumwita kutokana na usumbufu wa kukwepa kutamka jina hilo lililorefu si haba, ni msichana mrembo mno kutoka katika familia ya kitajiri, baba yake mzazi mzee shah-zomar ambaye alifariki miaka mingi kipindi tiffa akiwa bado ni mwanafunzi wa elimu ya upili, alikuwa ni mwanasiasa nguli mno katika nchi ya zambe na umahili wake katika kujieleza na kutetea wananchi aliweza kutunukiwa mara kibao tena mfululizo ubunge katika moja ya jimbo katika mkoa wa kijazi magharibi mwa nchi hiyo ya zambe.

    Kupelekea misimamo ya kisiasa ya m zee huyo hasa linapokuja swala la haki basi mzee shah-zomar aliuwawa kwa kifo cha risasi kutoka mikononi mwa kundi la watu wasiojulikana, japokuwa kifo chake kilihusianishwa na Imani za kisiasa lakini hakuweza kujulikana ni nani aliyefanya mauaji hayo mpaka kesi ilipofungwa.

    Uchungu wa kifo cha baba yake huyo pamoja na maapizo ya kulipiza kisasi msukumo mkubwa wa kujiunga na jeshi la wananchi ulimjia kichwani mwanadada Ashey-tiffa, kwani hakuona njia ingine ya kuweza kulipiza kisasi bali ni kuingia katika jeshi hilo. Msukumo huo ulimjia mara baada ya kumgundua aliyesababisha kifo cha baba yake si mwingine ni mkuu wa majeshi ya usalama ndugu jenerali HOMBABE.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Katika kumbukumbu zake mara kibao alimshuhudia jenerali huyo ambaye kipindi hiko alikuwa ni luternant wa jeshi hilo akimpa vitisho baba yake vya kufupisha Maisha yake na majibizano yalioonesha kutokuwa na hali ya Amani yaliendelea baina yao. Na hata kubwa Zaidi lililompelekea kukiri moyoni kuwa jenerali huyo anahusika na kifo cha baba yake ni ile hali ya jenerali huyo kutokea katika eneo la mauaji dakika chache baada ya kifo cha mzee shah-zomar huku bila kujua kuwa ameonwa na mwanadada huyo.

    Basi alikaa nalo rohoni kuhusu kumuhusianisha jenerali HAMBABE na mauaji ya baba yake mzazi na alipoamua kumueleza mama yake, mama ake huyo alimsihi anyamaze kwani yule ni kiongozi katika jeshi kwahiyo anaweza kumuua kabla kesi haijafikishwa mahakamani. Ashey-tiffa alibaki na uchungu moyoni huku akijiapiza lazima siku akutane na afande huyo na kuweza kulipiza kisasi.

    Hivyo akafanikiwa kujiunga na jeshi hilo mara baada ya kufanikiwa kupata shahada ya uzamili katika kozi ya public finance. Hakuchukua muda akafanikiwa kumaliza mafunzo yake na kufanikiwa kupata cheo cha uofisa. Kwa jitihada na ushupavu wa hali ya juu anajibidisha katika kujiimarisha kimwili ili lengo lake litimie. Lengo lake ni kuweza kupanda vyeo na hatimaye kumfikia jenerali HAMBABE ambaye ndiye alikuwa nafasi ya juu katika jeshi hilo.

    Ashey-tiffa anafanikiwa kukutana na D’oen katika kikosi alichopangiwa na katika hali isiyotegemewa, Ashey anapata msukumo moyoni mwake na kujiambia “huyu ndiye mtu ambaye anaweza kunisaidia kuweza kutimiza mipango yangu ya kuweza kumwangamiza yule mwanaharamu” anajisemea huku akiwa ameganda kumkodolea macho D’oen baada ya kumuona kaka huyo katika bwalo la maofisa akijipatia msosi katika moja ya meza ndani ya jengo hilo.

    Sijui ni kwanini mwanadada tiffa alipata msukumo na kufikia hatua ya kutamka maneno hayo? Je anamfahamu D’oen mpaka aamini kuwa huyo ndiye mtu atakayemsaidia kutimiza mipango yake? Bado ni swali lililokosa jibu.





    Akamsogelea na kuketi katika moja ya kiti pembeni ya meza hiyo ambapo D’oen aliketi na Hance wakipata msosi.

    Walipomuona tu walisimama na kumpigia saluti. Japo wote walikuwa ni maofisa lakini mwanadada Ashey-tiffa aliwazidi cheo.

    Akapokea salamu hiyo ya kijeshi na kuwaruhusu waketi.

    “hamjambo maafande” tiffa akaanzisha mazungumzo

    “hatujambo,vipi kwema afande?” D’oen akaitikia salamu ya mwanadada huyo huku nay eye akiuliza

    “salama, hivi nakuonaga onaga afande unaitwa nani na unapatikana combania gani?” tiffa aliongea kumwangalia D’oen huku akiwa amejawa na bashasha.

    “mi naitwa luteinant E.N. D’oen lakini ukiniita D sio mbaya, nipo combania ya bravo!” oen alijibu huku akiacha kula kwa muda.

    “oooh sawa basi mi ntaita D na nilivyo mvivu hivi” tiiffa aliongea na kufanya maafande wenzie wacheke,”enhee na wewe afande waitwa nani?” akahoji tena kumwelekezea swali hilo Hance.

    “officer cadet M.K.Hance”

    “ooh nice meeting you guys!” aliongea akiwapatia mikono kwa zamu,”mimi naitwa captain Ashey-tiffa S.T” naye akajitambulisha

    “ooh tunashukuru kukufahamu” hance na D’oen wakajibu kwa pamoja.

    Basi nae akaanza kula msosi mara baada ya kuletewa na wahudumu wa bwalo hilo.



    ****



    Maisha yalizidi kuendelea huku tiffa akiwa amejenga ukaribu kabisa na D’oen pamoja na hance lakini san asana alitokea kumzoea D’oen na baada ya kumchunguza na kuhakikisha ni mwanajeshi wa kawaida na si wale wanaoitwa maspy hivyo akaamua amweleze lengo la kuunda urafiki nae kwamba anahitaji amsaidie kulipiza kisasi cha baba yake.

    D’oen aliliunga mkono kimoyoni swala hilo la kulipiza kisasi ambapo liliendana kabisa na dhamira ya y eye kujiunga na jeshi hilo ambapo ni kuikomboa nchi kutoka mikononi mwa viongozi wanaojali masilahi yao kuliko maslahi ya umma.

    D’oen hakutaka kumuonesha kuwa nay eye lengo lake linafanana sana na lengo la mwanadada huyo kwa kuogopa inaweza ikawa mwanadada huyo amekuja ki mtego. Hivyo hapo awali alijifanya kumgomea lakini mwanadada huyo hakukata tamaa na wazi alionesha hiyo ilikuwa ni shida yake kweli.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Baada ya D’oen kumchunguza akagundua kweli mwanadada huyo si miongoni mwa mashushushu wa kijeshi akaamua kumkubalia kufanya nae kazi.

    Hivyo mipango ya chini kwa chini ya watu wawili ya kumpindua kiongozi huyo wa majeshi ikaanza!

    Mipango yao ikiwa inaendelea bahati mbaya ama nzuri yote inaweza ikawa kwa pamoja, bwana D’oen akafanikiwa kutajwa mmoja ya wanajeshi walioteuliwa kwenda kusomea kozi ya ukomandoo.

    Hiyo ilikuwa hatua moja wapo iliyoungwa mkono na D’oen kwani alijua atakaporudi huko hatokuwa mwanajeshi wa mchezo mchezo ambapo inaaminika komandoo mmoja huwa na nguvu za ziada za kupambana na akari wa kawaida yaan private wanne.

    Japo kwa mwanadada tiffa kwake hazikuwa taarifa njema kwani aliona mipango yake ya kumuangamiza kiongozi yule itachelewa,D’oen akampa moyo kuwa akirudi wataifanya kazi hiyo tena kwa wepesi wa hali ya juu.

    Hakukuwa na ziada Zaidi ya kuruhusu safari hiyo nyingine ya kijana huyo kufikia malengo yao.

    Hivyo akaambatana na makamanda wengine nane nay eye kuwa wa tisa na kuianza safari ya kwenda kuchukua kozi hiyo hatari nje ya nchi yao.

    Ashey-tiffa alibaki akimwombea mungu arudi salama ili mipango yake itimie.



    ****

    NDANI YA JENGO LA IKULU YA ZAMBE.

    Katika jengo hilo hali ikiwa imetulia kijana Alberto Banguli anaonekana akipitia baadhi ya mikataba kwa ajili ya rais kuweza kusaini. Yeye ndiye amebaki kuwa rais katika nchi hiyo na chochote hakipitishwi mpaka yeye hatoe amri, na vijana katika chama chake waliotokea kumpinga cha moto walikiona, iweje wao waache ikiwa rais mwenye mamlaka makuu hawezi kusema lolote? Basi wakabaki midomo kimya wakiugumia moyoni ama kutukania chooni mpaka hasira zao ziishe bila kumuathiri kijana huyo aliyeamua kupokonya nguvu yote ya nchi.

    Rais alitamani asingemsikiliza kijana huyo kipindi anampangia watu wa kuwaeka katika sekta nyeti ya ulinzi, laiti angelijua lililomoyoni mwa kijana huyo basi asingekubali lakini waapi ilibaki kuwa majuto ni mjukuu, kujuta hakukumfanya Alberto aweze kuiachia nchi hiyo mikononi mwake.

    Aliwaonea huruma sana wananchi wake ambao Dhahiri walikuwa wanateseka na serikali ilikuwa ikilijua hilo lakini lilifukiwa kama maiti ndani ya kaburi. Kuna muda rais machozi yalimtoka kila alipozipitia clip zake zilizorekodiwa kipindi akiomba kura kwa ahadi kemkem kwenda kwa wananchi wake.

    “shika hizi saini hapa” bwana banguli aliongea akimkabidhi karatasi hizo rais

    Rais alizichukua karatasi hizo na kujaribu kuzipitia kusoma kuhakikisha zina uhalali wa kusainiwa yeye.

    “hakuna haja ya kusoma, sijakuambia usome nimesema weka saini tu” banguli aliongea kwa ukali kumropokea rais wake.

    Mhe.dkt.Elias Stamphord hakuwa na namna Zaidi ya kukubali kusaini karatasi hizo bila kujua kilichopo ndani, angekataaje na wakati aliyempa amri ndiye mkubwa wake kwa wakati huo? Akasaini.

    Hakuyaamini macho yake kilichofuatia siku ya pili baada ya kusaini kwake kule.

    Alishuhudia hotuba fupi ya msemaji mkuu wa ikulu akielezea mkataba ule uliosemeka kwamba rais amekubali kufanya kazi na kampuni ya ujenzi ya TAKIU. Macho yalimtoka pima na bila wasi alionesha kushtusha na kile alichokuwa akikisikia na kukiona.

    “kwanini lakini banguli amekubali kufanya kazi na kampuni hii ambayo bungeni inapingwa vikali na wabunge pande zote? Oooh my god stamphord mimi nimekwisha!!!” alijisemea rais huku presha ikimpanda kwa kasi na jasho likimchuruzika kwa kasi kuelekea sehemu mbali mbali za mwikli wake.

    TAKIU ni kampuni binafsi inayojihusisha na ujenzi wa barabara, kutokana na sifa mbaya za ufisadi na utengenezaji wa barabara zisizo na viwango kampuni hiyo ilipigiwa kelele bungeni na hatimaye kufutiwa kibali cha usajiri. Masikini kumbe nyuma ya umiliki wa kampuni ile alikuwepo kijana Banguli ambaye ndiye waziri wa mambo ya ndani. Alivumilia kwa muda mrefu kampuni yake kupigwa marufuku lakini hakuweza kuvumilia tena pale alipoikamata nchi na kuamua analolitaka. Hivyo kupitia kivuli cha rais akamlazimisha rais asaini mkataba na kampuni hiyo katika kufanya nayo kazi ndani ya taifa lao. Kiulaini akafanikiwa kuirudisha kampuni hiyo katika chati.

    Unafikiri mhe. Dkt. Stanford angefanyaje kama si kupandwa na presha kwa kuona kwa macho yake nchi ikiharibiwa huku wananchi na watumishi wasiojua siri hiyo wakijua yeye ndiye mfanyaji? Hakuwa na chaguzi Zaidi ya kukasirikia nyuma ya Banguli kwa kuhofia kifo chake.

    Akajiushtukia akipiga ngumi iliyokunjwa kupitia mkono wake wa kushoto katika meza ya kioo iliyopo ndani ya chumba alichopo katika jumba hilo tukufu.

    Damu ndo pekee zilizokuwa zikimchuruzika kutoka katika mkono huo. Kipindi akiwa anataka kuunyanyua mkono huo kwa ajili ya kupiga tena ndipo wasaidizi wake pamoja na walinzi wakamuwahi kwa kumzuia asiendelee kufanya hilo alilolikusudia.

    “niacheniiiiii niacheniiiiiiiiiiiiiii” mhe.dkt. stamphord alibwata kwa nguvu kuwasambaratisha walinzi hao mikononi mwake.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wakasogea nyuma na kumshangaa!

    “mnanikamataaa eeee” akauliza kwa jazba,” nyie ni watu gani ee, ni watu gani ambao ni wanafiki, hivi mimi ndiye rais au yule kibaraka? Si nawauliza kwanini mnanizuia wakati kipindi nanyanyaswa nyie mnaniangalia tu, si mniache sasa nijiue, sioni umuhimu wangu wa kuishi ikulu,siooooni!!!” dkt. Stanford aliongea kwa jazba huku akimalizia kwa kilio na kujiegemeza kwenye moja ya kiti chumbani humo.

    “boss!” mlinzi mmoja akaita,” ni kweli usemayo lakini hatuna jinsi,angalia majeshi yote yapok wake tena watu ambao anafanya nao kazi vizuri hata mkubwa wa majeshi ya ulinzi na usalama, sasa sisi ni nani wa kuweza kumzuia?” aliongea kijana huyo kwa staili ya kuuliza swali.

    Dkt. Stamphord akabaki kimya akilia kwa kwikwi.

    “ulikosea mwenyewe mkuu kwa kumwamini kijana wako” mwengine aliongezea kuongea.

    Mhe. Dkt, Stanford aliendelea kuvuja damu kwenye ule mkono wake na taratibu nguvu zikaanza kumuisha na kujikuta akidondoka chini.

    Madakatari ndio walihusika mahali hapo na kumchukua kwa ajili ya kumpeleka kwenda kutibiwa katika chumba maalum.

    Taarifa zile za kuumia kwa rais na chanzo cha kufanya hivyo zilimfikia kijana mdogo aliyeamua kuitawala nchi ya zambe katika hali isiyopendezwa na katiba ya nchi hiyo, Alberto Banguli akiwa katika ofisi yake ya uwaziri.

    Alifurahi sana na baada ya kicheko chake hicho alichukua watu wake (walinzi) na kuanza safari kuelekea katika jengo apatikanalo raisi yaani ikulu.



    Ikiwa jua lililotoa mwale wa kichovu likiashiria kukaribia kuzama kwa jua hilo,Msafara wake uliokuwa ni mkubwa mno tofauti na inavyotakiwa kuwa kama waziri uliingia barabarani kuitafuta nyumba hiyo tukufu ya rais,

    ile picha ya urais ilijengeka kwake na hakuna aliyemuhoji kufanya hivyo kwani viongozi wengine wote alishawapiga mkwara na walibaki wakimtazama pasipo na kusema wala kufanya lolote Zaidi tu walibaki wakimsifia hata pale alipokuwa akikosea.

    *****



    Wakati huo huo Mwanadada maarufu katika jiji la ntovo ambaye ni mwanamke mwenye uwezo wa kutumia staili mbalimbali linapokuja swala la kucheza mziki kwa kutumia mwili wake ambaye bar ya kismart ndio iliyogundua kipaji chake kwa kumuajiri kama mchezaji na mburudishaji wateja, mrembo Zarish anapokea ujumbe kutoka kwa bosi wake mara baada ya kumaliza kutoa burudani hiyo ndani ya bar hiyo maarufu inayotumiwa na watu mbalimbali.

    Akapokea ujumbe huo ambao umefungwa ndani ya bahasha

    “imetoka kwa nani boss?” akahoji akionesha furaha

    “aah utasoma humo ndani na ukimaliza leo nakupa ofa, kazi yako imeisha tukutane kesho” boss wake aliongea huku akionesha bashasha na kumkabidhi kiasi cha pesa kwa ajili ya nauli kama makubaliano yao yanavyosema. Japokuwa muda wa kazi wa dada huo huwa ni kuanzia saa kumi jioni hadi saa tisa lakini siku hiyo boss alimwambia amempa ofa yaani amemruhusu aende mapema nyumnbani.

    Akafurahi na kuelekea moja ya chumba cha bar hiyo kwa ajili ya kujisafisha na kuvaa nguo za kawaida kwa ajili ya safari ya kurudi NYUMBANI kwake NDONI ambapo amepangiwa apartment na mbunge mmoja katika bunge la nchi hiyo.

    Anaingia chumbani humo na kuketi kitandani!

    Anaifungua bahasha hiyo na kukutana na barua ndani yake.

    Akatabasamu baada ya kukuta imepambwa vizuri.

    Akaanza kuikunjua tayari kwa kusoma!

    “HABARI, NILIFURAHI SANA SIKU YA KWANZA NILIPOTEMBELEA NDANI YA BAR HIYO YA KISMART NA NILIPOKUONA UKIBURUDISHA NILIINJOI SANA NILIKUKUTA WEWE UKITOA BURUDANI KWA KUUCHEZESHA MWILI WAKO VYEMA” Zarish akatabasamu kidogo baada ya maneno hayo y7a awali kisha akaendelea,”NA KUSEMA KWELI UMEJAALIWA SANA TENA SANA HASA LINAPOKUJA SWALA LA KUTUMIA KIUNO CHAKO. AYA TUACHANE NA HAYO, NILITAMANI SANA SIKU NILIYOKUONA NIONGEE NA WEWE HATA MARA MOJA LAKINI MUDA HAUKURUHUSU NA KAMA UNAVYOJUA WADHIFA WANGU NINAKUWA NA WALINZI KWAHIYO SI RAHISI KUKAA MUDA MREFU SEHEMU KAMA HIZO BILA WALINZI” moyo wa Zarish ulianza kumuenda mbio mara baada ya kulisoma neno wadhifa, hofu ya kutaka kujua barua hiyo imetoka kwa nani ikamuingia kama vile sindano ya clistapeni itiririshapo maumivu kwenye mishipa ya mwili. Akaendelea, “KWAHIYO NAKUOMBA USIKU WA LEO UJE NYUMBANI KWANGU USIKU NINAHITAJI BURUDANI AS VILE MIMI NI MPENZI WA BURUDANI ZAKO. WAKO MHESHIMIWA ALBERTO BANGULI” CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “ooooooh my god” Zarish akaonesha kutohamini baada ya kumalizia meseji ile na kuona jina la mtu aliyemuita, ni alberto waziri wa mambo ya ndani.

    Alijipepea kwa viganja vyake vya mikono kuonesha kutohamini. Akajiandaa upesi upesi kwa ajili ya kwenda nyumbani kwa mheshimiwa huyo.

    “boss mbona amenipa ofa leo atakuwa ameisoma nini hii barua” alijisemea huku akitabasamu.

    Alipomaliza kujiandaa alienda kumuaga boss wake na kuondoka. Neno kazi njema kutoka kwa boss wake aliyeonesha bashasha lilionesha wazi boss alikuwa anaijua fika ile safari na n do hapo akaelewa maana ya kupewa ofa siku hiyo.

    Kuna baadhi ya wanamume waliokuwa wakimuita siku hiyo kwa ajili ya kuburudika nao kama afanyavyo siku zote, aliwakacha kwa kuwapungia mikono juu juu na kuishia zake kuelekea nyumbani kwa waziri huyo.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog