Search This Blog

Sunday 22 May 2022

TAALUMA ILIYOPOTEA - 2

 





    Simulizi : Taaluma Iliyopotea

    Sehemu Ya Pili (2)

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “asante sana mzee, sina cha kukulipa ila naamini mungu atakulipa” nilimshukuru huku machozi yakinitoka, niliwaza sana ni kwanini nataseka kiasi kile na bado naendelea kuwa hai,,nilijiuliza sana kwanini nilistahili mateso yale.



    “nataka unielezee historia ya maisha yako na Natasha ni nani kwakuwa kila mara ulipokuwa ukishtuka ulikuwa ukimtaja mtu anayeitwa Natasha”,Mzee Russel alinitonesha kidonda cha siku nyingi ambacho japo hakijapona lakini nilianza kuyazoea maumivu yake lakini sikuwa na la kufanya zaidi ya kumueleza.



    “Mzee mimi nilizaliwa miaka 34 iliyopita nchini Tanzania, nilisoma huko mpaka kidato cha sita na baadae nilifanikiwa kujiunga na chuo fulani kinaitwa Mzumbe ambacho kipo hukohuko, nikiwa mwaka wa kwanza nilikuwa nikisomeshwa kwa mkopo wa serikali na fedha kidogo toka kwa familia yangu, mwezi wa 12 mwaka huo ikiwa ndio kwanza nina miezi mitatu toka nijiunge na chuo hicho nilikutana na msichana anaitwa Natasha katika mjadala wa wadau wa elimu na wanafunzi uliofanyika jijini Dar es Salaam hukohuko Tanzania, nilikuwa mmoja wa wachangiaji na yeye pia alikuwa ni mmoja wa wachangiaji,,baada ya pale nilifanikiwa kuongea nae na alinieleza kuwa alikuwa kidato cha sita shule ya Mt. Francis iliyopo mkoa wa Mbeya hukohuko Tanzania, kwakuwa alikuwa



    likizo aliweza kunipa namba yake na tulianza kuwasiliana. Kipindi hicho ndipo baba yangu alifariki na muda mfupi baadaye mama yangu naye alifariki hivyo nilibaki mimi na mdogo wangu tu, tulifukuzwa kwenye ile nyumba tuliyokuwa tukiishii kwakuwa ilikuwa ni nyumba ya kampuni, hivyo nililazimika kwenda kuishi sehemu inaitwa Tandale, eneo hili wanaishi watu wengi ambao maisha yao ni ya chini sana,,Natasha alinisaidia sana katika kipindi hiki nakumbuka hata pesa ya kwenda kupanda chumba huko ni yeye alinipa. Baada ya kumaliza mambo yote na kuhakikisha kuwa mambo yalikuwa sawa nilirejea chuoni na Natasha alikuwa amesharejea shuleni na hatukuwa na mawasiliano tena. Maisha yaliendelea na nilitumia pesa ile ya mkopo kwa kumsomesha mdogo wangu aliyekuwa kidato cha pili na pia kulipia ada yangu na matumizi mengine. Baadaye nilipokuwa likizo Natasha naye alikuwa amemaliza shule na alikuwa akija kunitembelea mara nyingi wakati nikiwa nyumbani,,sikuwa nimefahamu Natasha ni mtoto wa nani,,mara zote alikuwa akija kunitembelea na magari ya kifahari lakini kila nilipomuuliza kuhusu yeye hakunijibu,,alikuwa akiniletea vitu vya kutumia nyumbani pale na mwisho wa siku Natasha aliniomba nihame eneo lile na kuamia kimara ambapo alinisaidia kupanga nyumba ya vyumba viwili na sebule,,kila mara nilikuwa nikimuuliza ni wapi alikuwa anapata pesa lakini hakusema,,,baada ya kukaa kama marafiki kwa kipindi kirefu nilianza kumpenda Natasha na yeye alianza kunipenda,,nakumbuka alianza chuo kikuu cha Dar es Salaam akisomea shahada ya kwanza ya Ushirikiano wa Kimataifa. Baada ya kuanza mahusiano na Natasha maisha ya furaha yalinirudia lakini huzuni ilikuja kunirudia wakati nikiwa mwaka watatu ambapo mdogo wangu kipenzi aliyekuwa amebakia alifariki tena kwa kutoa ujauzito,,katika maisha yangu hasa baada ya kifo cha wazazi wangu Janeth ndiye mtu pekee

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    aliyekuwa amebaki katika maisha yangu,,nilimpenda na kufanya kila niwezalo ili asiishi kwenye vishawishi lakini sijui aliteleza wapi mpaka kupata ujauzito kisha aliutoa kienyeji na kizazi kilioza ndipo umauti ulipomkuta,,nilimshukuru mungu kwa kila jambo lililotokea katika maisha yangu na sasa nilijikita katika kumalizia masomo yangu ya sheria,,,nilibahatika kumaliza chuo na kutunukiwa shahada ya kwanza ya sheria, hii ilikuwa furaha kubwa sana kwenye maisha yangu, lakini mtihani mkubwa ulikuwa ni namna ya kumaliza masomo yangu ya uwakili niliyotakiwa kuyafanya mbeleni,,sikuwa na ada. Nakumbuka sikumoja nilimweleza Natasha juu ya nia yangu hiyo;



    “Natasha nahisi nitashindwa kwenda Law school kwakuwa kwasasa sina namna nyingine, ni bora nikakaa nitafute kazi” nilimueleza Natasha siku alipokuja kunitembelea nyumbani.



    “Si nilisikia mnapataga mikopo toka wizara ya katiba na sheria au?” aliniuliza





    “ndio ila mkopo kwangu ushakuwa mkubwa sana mpenzi,,mpaka sasa nadaiwa zaidi ya milioni tano na hawa bodi ya mkopo na sina kabisa namna ya kuongeza deni jipya” nilimuambia kwa sauti ya kukata tamaa.



    “okey basi nenda kachukue fomu, jaza na tutasaidiana namna ya kulipa” alinieleza kama vile alikuwa na uhakika wa kulipa.



    “Natasha nataka unieleze leo ni wapi unatoaga fedha za kunisaidia na wazazi wako wanafanya kazi gani” nilimgeukia na kumuuliza nikiwa na macho ya msisitizo.



    “okey, mimi naitwa Natasha Rweikaza” aliniambia huku akicheka.





    “hilo najua, mi ninachotaka kujua ni kuhusu familia yako” nilimuuliza huku nikionekana





    kuwa nilitaka kweli kufahamu,,,kilichonifanya nisimjue Natasha mpaka wakati huo ni masihara yake,,hakupenda sana nijue kuhusu kwao kwaiyo kila mara nilipomuuliza alinijibu utani tu.



    “mimi ni mtoto wa Robert Rweikaza” alinijibu huku akicheka.





    “acha masihara wewe,,huyu Robert Rweikaza ninayemfahamu mimi” nilinyanyuka nakukaa vizuri, nilishtushwa na taarifa ile kwani nilianza kumsikia Robert Rweikaza kipindi alipokuwa waziri wa habari na kulifungia gazeti la FIKRA lililokuwa likiandika mambo ambayo hayakuipendeza serikali, mzee Robert kabla ya hapo alikuwa ni Brigedia wa Jeshi la Wananchi na baadae aliacha na kujiingiza kwenye siasa kupitia chama cha wakombozi na kufanikiwa kuwa mbunge wa Nsimbi kabla ya kuchaguliwa kuwa waziri wa habari,,wengi walimuita wembe kwakuwa kila aliyeonekana kuigusa serikali basi alimkata au kumnyamazisha,,japo alipendwa kwakuwa alikuwa mtu wa kujichanganya na alijali matatizo ya watu,,kwa wakati huo nikiwa na Natasha baba yake alikuwa ni balozi wa Tanzania nchini Cuba na ni moja ya watu waliokuwa wanatajwa kuja kugombea urais siku moja.





    ***



    Nilisomea uwakili na kufanikiwa kumaliza baada ya kupata mkopo kutoka wizara ya katiba na sheria na baadaye nilijiunga na chuo kikuu cha Pretoria huko Afrika ya kusini kwaajili ya shahada ya pili,, kama sio Natasha nisingeweza kusoma shahada ya pili kwakuwa yeye ndiye aliyenilipia kila kitu wakati huo yeye alikuwa ameshamaliza chuo na alikuwa



    akifanya kazi wizara ya mambo ya nje. Nilianza kufanya kazi kwenye kampuni ya wanasheria kwa kujishikiza lakini muda sio mrefu ndoto zangu zilianza kufifia.



    Uchaguzi mkuu ulikuwa umefika na sasa ilikuwa ni kipindi cha kumchagua rais na wabunge,,kipindi ambacho katika maisha yangu sitakisahau,,mapenzi yangu na Natasha yalikuwa yamepamba moto,,na alikuwa akipanga kunipeleka kwa wazazi wake ili kunitambulisha,,wakati huo Robert Rweikaza alikuwa ameteuliwa na chama chake kugombe urais wa nchi hiyo,,hivyo Natasha alikuwa sasa akilindwa kila alipokuwepo na namna ya kuonana nae ilikuwa ni ngumu. Nakumbuka kuna siku aliwatoroka walinzi wake alipokuwa akitoka kazini na kuamua kuja kwangu, na alipoondoka aliniachia kiasi fulani cha pesa lakini baada kama ya masaa mawili ziliingia gari tatu nyeusi na watu waliovalia suti nyeusi na miwani nyeusi walifika pale na kuingia kwangu bila kugonga hodi na mmoja alinifata na kunipiga teke la tumbo:

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “kijana kaa mbali na Natasha si wa hadhi yako, tutakupa onyo mara tatu tu,,hii ni ya kwanza, umebakiza mara mbili,,,yule ni mtoto wa mtu mkubwa anayekaribia kushika dola kwa sasa,,hawezi kuwa na mtu unayeishi kwenye mazingira kama haya,,,kaa mbali naye hatutakuonya zaidi ya mara tatu” aliniambia hayo na taratibu waliondoka na kuniacha bado nikivumilia maumivu ya tumbo pale,,nilinyanyua simu na kumpigia Natasha lakini hata yeye hakuelewa wala kuwatambua watu hao,,nilimtajia aina za gari zilizokuja pale na alionekana kufaham kisha alikata simu na aliponipigia simu baadaye alikuwa akilia:



    “siko tayari kukuacha Frank, haijalishi ni nini kitatokea kwenye maisha yangu” aliniambia hivyo na mimi sikumuelewa.



    “unamaanisha nini?” nilimuuliza na ndipo aliponiambia kuwa familia yake imegundua mahusiano yetu na kuwa alinilipia ada na pesa amekuwa akinipa mara nyingi hivyo wamemwambia aachane na mimi kabisa. Sio tu yeye alikuwa hayuko tayari kuachana na mimi ila hata mimi sikuwa tayari kuachana naye, sio kwasababu ya hadhi yake au ya familia yake ila kwa mapenzi aliyonionyesha,,,niliamini kabisa yeye ndiye mwanamke wa maisha yangu, hata angekuwa katika hali gani ya maisha ningemkubali. Maisha ya vitisho yaliendelea wakati kampeni zikiendelea.



    Siku moja asubuhi nikiwa kwenye daladala kuelekea mahakama ya hakimu mkazi kisutu nilishtuka baada ya kuona gazeti moja la udaku lililokuwa na kichwa cha habari MTOTO WA MGOMBEA URAIS NDANI YA SKENDO YA NGONO NA MUUZA MADAWA YA KULEVYA, kichwa hiki cha habari kilifuatiwa na picha chini yake iliyokuwa ikimuonyesha Natasha na nyingine ilinionyesha sura yangu,,nilinunua lile gazeti na kuamua kuahirisha safari yangu na kurudi ofisini,,nilipofika nilikaribishwa na barua ya kufukuzwa kazi. Nilishindwa kuelewa mambo yalivyokuwa yakienda, niliingia kwenye daladala mpaka nyumbani kwangu na kuanza kuisoma ile habari,,ilikuwa ni habari iliyokuwa imetengenezwa kwa ustadi wa aina yake na na haikuwa rahisi kwa mtu kukataa.



    Usiku wa siku hiyo nikiwa nyumbani nilisikia gari mbili zikiegeshwa pale nje, na kabla hata sijachungulia mlango ulipigwa teke na hapo waliingia vijana watatu kisha alifata mzee ambaye nilimtambua, alikuwa ni mzee Robert Rweikaza,, akinitupia lile gazeti;



    “Mzee si kweli,,hii ni habari ya kupikwa tu,,mimi ni mwanasheria mtiifu siwezi kufanya mambo yanayoweza kuhatarisha taaluma yangu mzee” nilimwambia hayo huku nikipiga



    magoti.





    “hahaaa,,,mwanasheria,,,wa chuo gani kijana?” aliniambia hayo huku akicheka na kabla sijajibu chochote alinisogelea na kunitazama kwa hasira.



    “kijana umeshaharibu kila kitu ulichokitengeneza toka ulipozaliwa,,umeharibu na sasa usitake kuharibu mambo yangu,,hii skendo itaniharibia kwenye uchaguzi wangu na sitakubali iniharibie mimi kabla ya kukuharibia wewe,,KAA MBALI NA BINTI YANGU hasa kwa kipindi hiki,,yule ni mtoto pekee wa kike niliye nae,,si wa hadhi yako,,,nakusihi kaa mbali nae kwakuwa PESA ITAOA PESA,,hili ni onyo la mwisho na nataka mpaka kesho uwe umeshamwambia Natasha kuwa humtaki na wewe uwe umehama hii Dar,,” alinyanyuka na kuingiza mkono mfukoni kisha alitoa pesa kiasi cha shilingi laki tano na kunirushia.



    “Nenda popote nje ya Dar ukaanze upya maisha yako” aliniambia na kuondoka,,sikujua nini cha kufanya,,usiku uleule nilimsikia akihojiwa juu ya ile skendo lakini alijibu kuwa mtoto wake hakuwa anamahusiano na mimi ila tu mimi nilikuwa nikitumiwa na wapinzani wake wa kisiasa waliotaka kumuangamiza..alienda mbele zaidi na kusema huyo kijana wamesema ni mwanasheria lakini si mwanasheria ni muhuni tu anayetumika kukwamisha uchaguzi wake.



    Kesho yake asubuhi nilipoamka nilienda tena mpaka kazini kutaka ufafanuzi wa kwanini nilifukuzwa kazi lakini nilishtuka kukutana na wito wa mahakama kujibu shtaka la kufanya kazi za sheria wakati mimi si mwanasheria,,nilishtuka na kurudi nyumbani ili kuweka vyeti vyangu sawa kama ushahidi lakini nilishangaa kukuta vyeti vile havipo,,niliingia kwenye mtandao na kutafuta jina langu kwa wahitimu waliomaliza Mzumbe kitivo cha sheria lakini







    niliambiwa jina hilo halitambuliki,,hata kwenye picha za wahitimu nilipotazama pale nilipokuwa mimi hapakuwa na picha yangu bali ua,,nilichanganyikiwa na kuingia kwenye tovuti ya Law schoof of Tanzania ambapo nako jina langu wala taarifa zangu hazikuwepo wala kwenye picha za wahitimu wa mwaka huo niliomaliza sikuwepo,,nilifungua tovuti ya Chuo kikuu cha Pretoria na huko nilikuta jina langu lakini inaonekana nilifeli na kufukuzwa chuo. Nilitafuta vyeti vyangu pale nilipoviweka lakini sikuviona hata nakala moja wala picha wala ktu chochote,,nilipiga simu ya Natasha lakini iliita bila kupokelewa.



    “Mapenzi ya kweli hudumu milele,,hila na chuki za kupandikizwa huweza kumfanya mtu adhani kuwa hawezi kabisa kupenda tena,,lakini mambo huwa tofauti, ukimpenda mtu kweli, haitajalisha umepata maumivu kiasi gani kwa kutoelewa kwake, utaendelea kumpenda huku ukimwomba mungu amfumbue macho. Kuna watu tunakutana nao katika maisha yetu na hutokea kuwa wathamani kwetu kwakuwa wanajali sana furaha yetu kuliko waliotufahamu kabla,,furaha zetu hurudi tena pale faraja ya kweli inapoambatana na moyo wa uvumilivu unaokumbatia matatizo yetu na kuyaficha tusiyaone..” KILA MTU NI WA MUHIMU KWAKO,,LISHA MBWA WOTE CHAKULA SAWA KWAKUWA HUJUI YUPI ATAKUOKOA SIKU YAKIKUFIKA”…HII NI SEHEMU YA NNE,,,,ANDIKA HIVI.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    ….Nilitafuta vyeti vyangu pale nilipoviweka lakini sikuviona hata nakala moja wala picha wala kitu chochote,,nilimpiga simu ya Natasha lakini iliita bila kupokelewa. Sikujua nielekee wapi na wala sikujua nifanye nini, nilitoka mpaka kilabu cha pombe kilichokuwa karibu na pale nyumbani na kuanza kunywa pombe, yote ni kuamini kuwa ningeondoa mawazo lakini haikuwa hivyo, nilikuwa nimeahirisha mawazo kwa muda tu na nilipoamka kesho yake asubuhi hakika bado mawazo yalinisonga,,,nilitoa kila kitu nje ya kile chumba lakini sikuona hata karatasi moja iliyokuwa na dalili hata ya nakala ya cheti changu. Niliondoka pale nyumbani na kwenda kituo cha mabasi cha ubungo nikakata tiketi ya kwenda morogoro, nilipanda gari majira ya saa nne na ndani ya masaa mawili nilifika kituo cha basi cha msamvu pale morogoro, wakati na shuka nilifanikiwa kukutana na Abdulaziz kijana wa kipemba niliyesoma nae darasa moja,;

    “Bora nimekuona Abdul,,za masiku kaka?” nilimuuliza huku kabisa nikionekana kuwa sikuwa sawa.

    “Salama kijana,,mbona unaonekana umechoka sana na mkanda hujavaa, uko sawa kweli” aliniuliza huku akinitazama huku na huku”

    “Siko sawa Abdu, nina matatizo makubwa sana ambayo si rahisi kuyaelezea” nilimueleza na hivyo na kumvuta pembeni,,kabla sijamuambia chochote nilijikuta machozi yakinitoka,,dhuluma ninayofanyiwa haikuwa sahihi kabisa, ni umafia na si kitu kingine,,nililia kwakuwa nilihangaika sana mpaka kupata elimu niliyokuwa nayo ambayo kwasasa sina ushahidi nayo, nililia sana kwasababu pamoja na kuwa nilimpenda mtoto wa kigogo lakini mapenzi yangu kwake hayakuwa kwasababu ya hadhi aliyokuwa nayo baba yake,,na kuwa kwenye mahusiano na mwanae halikuwa kosa kubwa lililostahili mimi kunyang’anywa elimu niliyoisumbukia siku zote za uhai wangu, halikuwa kosa kubwa namna ile.



    “Najua hauko sawa” nilishtushwa na kauli hiyo ya Abdu na kujikuta nikitoka kwenye kuwaza na kurudi tena duniani.

    “unamaana gani?” nilimuuliza Abdu kwa shauku.

    “najua kuhusu taarifa iliyoandikwa kwenye gazeti,,lakini najua pia kuwa huna elimu ya chuo kikuu” aliongea yale maneno na kuonekana kama vile aliujua mpango wote.

    “Abdu unaelewa nini kuhusu hili?” nilimuuliza tena.

    “Najua kwa hapo tu nilipokuambia,,ujue Frank maisha si sawa na ambavyo unaweza ukadhani, kuambiwa sisi sote ni sawa usidhani ni sawa hapa duniani,,hapana, sisi ni sawa mbinguni, hapa duniani tunatakiwa tuishi tukiifahamu sheria tu na si haki yetu, uifahamu sheria inakupa wajibu gani na si sheria inakupa haki gani, huo ndo msingi wa maisha ya binadamu. Unaweza kuwa una elimu kubwa sana, lakini elimu yako si kitu kwa mtu mwenye nguvu na madaraka, nchi hii inaongozwa na wenye nguvu sio wenye elimu,,mwenye elimu ni kibaraka tu wa mwenye nguvu hivyo jitahidi sikuzote kufata misingi ya mfumo mpya na si mfumo wa zamani, mapenzi yasizidi yakaharibu misingi ya sheria na wajibu wako kwa wenye nguvu, fedha haiendi pachafu, usafi wa nafsi haukutoshi wewe kujitwika taji la ufalme wa nyika ambayo si hadhi yako. Wahenga walikuwa na busara na utashi wa kiundani, ila walitahadharisha haya yanayokutokea waliposema,,kubali matatizo yakutafute ila si wewe uyatafute. Mchuma janga hula na wa kwao. Pole sana” hizo zilikuwa ngonjera tu kwangu, sikuelewa lolote alilolisema,,niliinama chini nikiwaza na kuwazua lakini nikaona ninaota, nilinyanyua kichwa ili kumuomba ushauri lakini sikumona pale nilipotazama mbele niliona akiwa ndani ya Land Rover Discovery huku akinipungia kuashiria kuwa alikuwa akiondoka.



    Nilipanda daladala pale msamvu na kushika njia kuelekea Mzumbe, muda wote kwenye gari nilikuwa nikiyatafakari maneno aliyoniambia Abdu, baada ya mwendo wa kilomita 20 tulikuwa tumefika Mzumbe, nilishuka na moja kwa moja nilielekea ofisi ya msajili na kuulizia taarifa zangu lakini walisema kuwa sitambuliki,,nilienda kutafuta walimu walionifundisha kipindi kile lakini sikumpata hata mmoja, nikaingia kwenye ofisi ya mkuu wa chuo na huko ndiko nilikokatishwa tama baada ya kuambiwa kuwa hawajawahi kuwa na mwanafunzi kama mimi pale chuoni. Nilitoka nje nakuhisi kama dunia sasa imenitenga,,sikuwa na la kusema licha tu ya la kufanya. Ilikuwa imeshafika majira ya saa tisa mchana, nilitafuta simu yangu ili niweze kumtafuta tena Natasha lakini haikuwepo, nilipofikiri zaidi niligundua kuwa nilikuwa nimeisahau nyumbani, nilipanda daladala pale na kuondoka tena mpaka msamvu kisha nilichukua basi na kurudi Dar, kwenye majira ya saa nne usiku nilikuwa nimeshafika nyumbani, akili ilinijia kichwani nitafute muhuri wangu,,ooh nilichoka nilipoukosa,,yani walikuwa wamechukua kila kitu.



    Nilikaa pale ndani nikiwa sina ramani yoyote ya maisha,,hakuna mahali ningeweza kwenda na nikasikilizwa, haki yangu haikutambulika popote tena na sasa nilibakiwa na hatia tu,,ikumbukwe kuwa hapa pamoja na mambo mengine bado nilifunguliwa kesi mahakamani ya kudanganya na kufanya kazi kwa taaluma nisiyokuwa nayo.

    Niliitafuta simu yangu nilipokuwa nimeiweka na kisha nilibahatika kuiona, nilikuta Natasha amepiga simu mara tisa na mwisho aliamua kutuma ujumbe uliosomeka ‘una matatizo gani?’, nilifarijika sana kukuta ujumbe ule kutoka kwa Natasha,,niliipiga namba yake lakini haikuwa inapatikana,,niliketi pale chini nikitafakari mpaka kulipokucha, sikuwa na usingizi wala njaa, kulipopambazuka niliamua kuondoka na kwenda wizara ya mambo ya nje ya nchi, nilipofika nilimuulizia Natasha na nikaelekezwa ofisini kwake. Baada ya kufika pale nilionana na katibu muktasi wake na kuniruhusu niingie ndani, nilipofungua tu mlango pamoja na kwamba pale ndani kulikuwa na mtu ambaye sikumfahamu ila nilimshuhudia Natasha akiacha alichokuwa akikifanya na kuja kunikumbatia,,nilifarijika sana na ile hali lakini haikuchukua muda nilinywea kama majani mbele ya jua, mlango ulikuwa umefunguliwa na aliingia baba yake pale ofisini. Nilipomtazama Natasha alionekana kumuogopa sana baba yake ingawaje alikuwa ni msichana mkubwa mwenye uwezo wa kujiamulia mambo yake. Nilimsalimia yule mzee na aliitika vizuri kama hakuna lililokuwa linaendelea, niliwapisha ofisini pale na muda kutoka nje, lakini cha kushangaza nilipotoka nje ya ile ofisi tu walifika maaskari pale na kunikamata;

    “uko chini ya ulinzi kwa kosa la kujihusisha na uuzaji wa madawa ya kulevya na kosa la kujaribu kumdhuru Natasha Rweikaza, una haki ya kunyamaza kimya na lolote utakaloongea litatumika dhidi yako mahakamani” hayo yalikuwa ni maneno machache tu waliyoongea wale maaskari na kunifunga pingu, nilibaki mdomo wazi na sikuelewa nini cha kusema, ghafla nikiwa pale nilimuona Natasha akitoka na baba yake huku machozi yakimtoka, alifika pale nilipo na kunipiga kofi;

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “haya ndo malipo ya wema wangu kwako Frank?” aliniuliza huku akiendelea kulia, nilikosa cha kujibu, yani kila kitu pale kilikuwa kinakwenda haraka na sikujua nijibu nini.

    “Natasha sio….”nilikatishwa na kofi linguine toka kwa Natasha.

    “Shut the fuck up, do you think am that idiot?huh, I spent my money, my love and my carreer just to make a better life with you but today you want to kill me?”(nyamaza, unadhani mimi ni chizi, nimetumia zangu, mapenzi yangu, na kazi yangu ili kutengeneza maisha mazuri na wewwe ila leo unataka kuniua). Aliniambia maneno yaliyonishtua lakini kabla sijajibu nilianza kupekuliwa na wale maaskari na huku Natasha akitazama kwa makini, nilipopekuliwa nilikutwa na bomba la sindano lenye dawa, nilianza kupiga kelele kuwa silitambui ilo bomba lakini hakuna aliyenisikiliza, si Natasha wala si mtu mwingine yeyote pale, Natasha alizidi kulia na baadaye aliondoka na mimi nilipakiwa kwenye gari ya polisi tayari kwa kuelekea kituo cha polisi ambapo jalada la kupanga kuua lilifunguliwa na kisha nilipakiwa kwenye gari hilohilo na kwenda kwangu kupekuliwa ambapo ilikutwa chupa ndogo mbili za sumu, bastola moja yenye risasi nane, kadi za ATM ambazo sikujua zimefikaje pamoja na madawa ya kulevya gramu 250 na pesa bandia laki 7, nilichoka kwakweli, sijawahi kuwa na hivyo vitu lakini pia viliwekwa kiustadi mkubwa sana na hakuna aliyeamini kuwa haikuwa kweli, majirani zangu pale wote walishtushwa na walianza kurusha mawe juu ya bati wakisema mtoeni huyo mwizi tumuue,,nilikuwa nikilia tu hasa ukizingatia nilikuwa nimeshapigwa na maaskari na mwili wangu ulitapakaa damu lakini sikujua nilichokuwa nikikifikiria, sikuwa na la kusema,,ilikuwa kama ndoto lakini kiuhalisia ilikuwa kweli kabisa, baada ya hayo yote nilipelekwa mahabusu na kesho yake nilifikishwa mahakamani, ambapo nilisomewa mashtaka nane, 1. Kujaribu kuua,,2. Kukutwa na silaha kinyume cha sheria,,3. Kukutwa na madawa a kulevya,,4. Kukutwa na fedha bandia,,5. Kuvamia ofisi ya mfanyakazi wa wizara ya mambo ya ndani,,6. Kufanya kazi za sheria wakat sikuwa na kibali cha kufanya hivyo,,7. Kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu na 8 ni kadi za benk kinyume na taratibu. Haya yote yalikuwa ni makosa yangu na sikuruhusiwa kujibu chochote mpaka uchunguzi utakapo kamilika,,,wakati natolewa nje ya mahakama na nilipoingizwa kwenye defender ya polisi nilimuona Natasha akija pale na akaruhusiwa kuongea na mimi..macho yake yalikuwa mekundu sana;



    “kama niliwahi kukuambia nakupenda na niko tayari kufanya lolote kwaajili yako basi leo hii nikuambie tu kuwa nakuchukia sana na niko tayari kufanya lolote kuhakikisha unaishi kwa mateso sana hapa duniani kama si kufa,,,ulikosa nini kwangu mpaka ukatumike na wanasiasa kupanga kumuumiza baba yangu kwa kuniua mimi,, nilikupa fedha ukasome kumbe hukuwa unasoma, nilidhani ulikuwa mwanasheria kweli kumbe tapeli tu,,nakuambia utajuta kwa hili” aliongea huku machozi yakizidi kumtoka.

    “Natasha sikiliza mpenzi” nilijaribu kujitetea lakini haikuwa hivyo kwani alikuwa ameshafunga ule mlango na kuondoka na baadaye nilirudishwa mahabusu,,wiki mbili mbele nilipelekwa pale mahakamani lakini kama vile naota nilisikia mwendesha mashtaka wa serikali aliamua kufuta mashtaka yale na niliachiwa huru, sikujua kuachiwa kwangu huru ulikuwa ni mchezo wa kiufundi uliokuwa unachezwa ili kumuonyesha Natasha kuwa kweli nilikuwa nikitumia na watu waliokuwa na nguvu sawa na baba yake. Baada ya kurudi nyumbani sikuiyo usiku niliamua kubeba vitu vyangu na kuhama kabisa eneo lile, nikaenda kuishi Kibaha kwenye kibanda cha udongo kilichokuwa kwenye shamba la marehemu babu yangu,,lakini mambo hayakuishia pale,,nilijitahidi kumtafuta Natasha ili nimueleweshe lakini sikufanikiwa kabisa, baada ya siku tatu nikiwa kwenye kibanda change nilisikia gari zikiegeshwa nje nilichomoka mbio lakini sikufika mbali nilisikia kitu kikipenya kwenye mguu wangu na kunifanya nikae chini, baada ya kutizama na kupata fahamu kuwa kuna mlio mkubwa nimeusikia nikagundua ilikuwa ni risasi, wakaja vijana watatu wakaanza kunipiga sana mpaka nikalegea kabisa kisha walinisogeza karibu na ile gari na hapo nikamuona Natasha;



    “nilikuahidi mateso kwa ulichonifanyia na sasa hayo ndo uyapatayo, umeniumiza sana, ulikuwa masikini wa kutupwa lakini nilijitolea kukupenda kumbe wewe una ajenda yako ya siri ya kuniangamiza, nilikupa kila kitu,,nilikuachia mwili wangu na kila nilichonacho, kila kitu kwangu ulipata,,ni bora ningekukuta na mwanamke mwingine lakini si wewe kupanga kuniua mimi” nilisikia akinisemesha,,nilijitahidi sana kujitetea lakini sikupewa nafasi, walimaliza kunipiga na kuniacha pale chini nikiwa nimelala bila msaada wowote,, nilianza kujivuta taratibu nikarudi tena mpaka kwenye kile kibanda change nikajilaza,,,asubuhi na mapemba niligundua kuwa siwezi kunyanyuka kwakuwa mbavu zilikuwa zinauma,,nilikaa bila kula kwa muda mrefu ila baadae nilianza kujivuta hadi nje,,nikasogea karibu na shina la muhogo na kuanza kuushimba taratibu, nilifanikiwa kupata kipande kimoja na kukipeleka mdomoni japo kilikuwa kichungu sana.



    Basi nilikaa katika hali hiyo kwa muda wa siku nne na nilianza kupata nafuu na siku ya tano usiku alikuja mzee Rweikaza na walinipakia kwenye gari huku wamenifunga kitambaa cheusi usoni, baada ya mwendo mrefu sana nilihisi nachomwa sindano na hapo sikuamka tena mpaka baadaye nilianza kusikia tena sauti ya watu wakijadili jambo Fulani na hapo nilipotaza nje niligundua ilikuwa ni uwanja wa ndege, wale watu baada ya mazungumzo na kupeana maelekezo hayo walikuja tena pale nilipokuwa mimi na sasa nilisikia wakiambiana mchome tena ya masaa 96, nilikaa kimya nikasikia tena sindano ikiingia mwilini mwangu na hapo mda mfupi mbele sikusikia chochote mpaka nilipokuja kuamka na kushangaa nikiwa ufukweni mwa bahari, nilipotazama huku na huku sikuona chochote zaidi ya boksi lililokuwa limechomekwa kwenye mti nyuma ya pale nilipokuwa kilichokuwa kimeandikwa kwa lugha ya kingereza iliyomaanisha,,usiongee Kiswahili kama unataka kuishi kwa Amani, tafuta maisha sahau ulikokuwa,,karibu Madagascar. Nilishtuka sana na nikaamka pale nilipokuwa nikaanza kutembea nisipopajua, baada ya mwendo mrefu nilikuwa tayari nina njaa na sikujua pa kupata chakula,,,nilivua shati langu na kuzama baharini ambapo nilibahatika kupata samaki mmoja nilirudi ufukweni na kukuta wavuvi wakisubiri muda wakuingia baharini ufike, niliomba kibiriti na kupatiwa kisha nikawasha moto na kumchoma yule samaki kisha nilikula. Kwakuwa sikupajua pale vizuri ilinibidi kulala kule ufukweni na kuishi huko kama sehemu ya maisha yangu mpaka nilipokuja kupata rafiki mvuvi ambaye hata hivyo sijawahi kumweleza chochote kuhusu mimi, nilianza kujifunza kuvua samaki na nilipoweza basi nilikuwa naingia mwenyewe baharini navua samaki na kuanza kuetembeza mitaani, hiyo ilikuwa kazi yangu kwa mda wote wa miaka mitano niliyojikuta nikiwa nchini Madagascar jiji la Antananarivo, uzoefu wangu na ukarimu wangu ulinifanya kupendwa na wengi na wakati huo nilikuwa bado nikikaa na kusoma pale nilipopata muda,,nilikuwa nikiandika kitabu change cha THE LOST PROFESSION kilichokuwa kinaelezea maisha yangu na kila kilichokuwa kinanitokea kwa siku za maisha yangu. Baadae nilikuja kupata kazi nyumbani kwa mzee Aristede Rusovelt na ndipo yaliponikuta mambo yaliyosababisha majeraha haya niliyoyapata.” Nilimaliza kumuhadithia Mzee Russel na nilipotazama niliona mkewe na mwanae wakilia.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “msilie, yamepita na nashukuru kwakuwa niko hai” niliwaambia huku nikitabasamu. Walinipa pole kwa pamoja na maisha mapya yalianza tena pale msituni, japo nilijua kuwa baba yake na Beatrice hata sita kunitafuta na kuniua kama atagundua bado nilikuwa hai. Kwakipindi chote hiki sikuwahi kumsahau au kuacha kumpenda Natasha, sikumlaumu kwa lolote kwakuwa hakufahamu ukweli bali uongo na dhuluma ilipandikizwa kwenye kichwa chake na kumfanya auamini, niliamini ipo siku moja ataujua ukweli na pengine tungeweza kuwa pamoja tena,,japo sikutegemea tena kurudisha kila nilichokipoteza.



    MWEZI MMOJA MBELE



    Nimepamis sana nyumbani, hilo lilikuwa wazo la kwanza kunijia kichwani siku iyo, niliamka na kuketi, mawazo yalinijaa na nilijiuliza nitakuwa mtumwa hadi lini,,nilisogea mpaka kwenye kioo na kujitazama vyema, nilikuwa na ndevu ndefu na uso wangu ulikuwa umebadilika kabisa, sio rahisi kwa mtu yoyote aliyeniona miaka mitano iliyopita kuweza kunitambua leo,,kutwa nzima mawazo yalikuwa ni kurudi nyumbani,, niliandika barua ndefu yenye kurasa sita kwa Beatrice nilimweleza kila kitu kuhusu mimi na kumtaarifu kuwa narudi Tanzania. Sikutaka kuondoka lakini niliona huu ndo muda wa kurudi nchini,,nirudi nikayatazame japo makaburi ya wazazi wangu na lile la mdogo wangu kabla sijafa. Baada ya kuandika ile barua nilimpatia mtoto wa mzee Russel aipeleke kwa kina Beatrice, nilimuelekeza kila kitu lakini nilimwambia akifika ampe mlinzi wa geti na asimwambie imetoka kwa nani, alienda mjini siku hiyo na alifanikiwa kuifikisha lakini alisema alipokuwa anagonga geti alitoka msichana Fulani na alimpatia lakini yule msichana hakuuliza chochote,,kwajinsi alivyonitajia kuhusu huyo msichana nilijua kuwa ni Beatrice.

    Jioni siku iyo baada ya chakula nilimueleza mzee Russell na mkewe juu ya nia yangu ya kutaka kurudi nchini kwangu na hivyo wao walianza kuniandalia namna ya kusafiri na baadaye walinipa kiasi cha pesa ili kinisaidie nitakapofika huku.

    ***

    Ni Septemba ya tarehe13 mwaka 2010 saa 9:45 jioni niliondoka nchini Madagascar kurejea Tanzania, nikiwa pale uwanja wa ndege wa Antananarivo ilikuwa huzuni na simanzi kwangu na kwa familia ya mzee Rusell, hao ni watu walionifanya nijione binadamu tena baada ya manyanyaso ya muda mrefu ya walimwengu, nilikuwa nimebadilika kabisa.



    “Maisha ni kama Shamba, wapo ambao wazazi wao walifanikiwa kununua shamba hili na wao kwa juhudi wazijuazo wao walifanikiwa kung’oa visiki, kulima, kupanda mbegu na kupalilia na kisha sasa mazao yanamea na wao wananyweshea,,watoto au vijana wenye wazazi wa namna hii huwa hawana kazi sana,wao huwapokea wazazi wao mpira wa maji na kuanza kumwagilia. Wapo wale ambao wazazi wao walifanikiwa kununua shamba lakini walishindwa kulihudumia na sasa wao ndio huenda kuanza upya, kazi yao huwa ngumu sana kwani hutakiwa kuanza mwanzo, hawa ni wale waliobahatika tu kupata elimu lakini kwao hakuna uwezo. Ewe ambaye kwenu mmefanikiwa usikatishe ndoto ya mwenzio kwa uwezo wa mzazi wako,,,USITUMIE PESA KAMA FIMBO YA KUMCHAPIA MWENZIO” HII NI SEHEMU YA TANO….ANDIKA HIVI



    **BEATRICE ANASIMULIA**



    “hapana mimi si muhalifu niacheni jamani” Frank alizidi kujitetea wakati wale maaskari wakizidi kumkunja pale chini , sikujali hilo kwakuwa bado sikutaka kumuona duniani.

    “ni muongo huyo mkamateni na mumtoe ili abiria wengine waendelee na safari yao” niliendelea kuwasihi wale maaskari ili wamkamate Frank na walifanikiwa kumchukua pale kisha tulishuka kwenye ile ndege na muda mfupi mbele ndege iliondoka, Frank alikuwa bado pale chini akilia lakini sikuwa na huruma naye;

    “Beatrice nipe muda nikuelezee ukweli wa kila kitu tafadhali, ni bado mapema sasa wewe kuujua ukweli, mimi si kama unavyodhani, mimi si muhalifu, historia ya maisha yang undo iliyonileta hapa nilipo” aliendelea kuongea na mimi lakini sikutaka kusikia tena uongo wake, nilichukua simu yangu na kumpigia baba yangu nikamtaarifu kuwa tayari nilikuwa niko na Frank pale na juhudi zake za kutoroka zilikuwa zimegonga mwamba. Nilimtazama Frank usoni alionekana kuchoka sana lakini swali kubwa kichwani ni alikuwa anatoroka kwenda wapi.

    “Beatrice” aliniita na mimi nilimsogelea mpaka pale alipokuwa huku nikimtazama kwa uso uliojaa chuki, sikumpenda tena Frank hasa baada ya kugundua kuwa hata jina lake alinificha toka mwanzo, nikiri leo kuwa ingawaje Frank alikuwa ni mfanyakazi wa ndani nyumbani kwetu ambaye kiuhalisia alikuwa hana hata hadhi ya kuwa rafiki yangu wa karibu lakini nilianza kuwa na hisia nae na niliuahidi moyo wangu kuwa ningembadilisha na kumfanya mwanaume mwenye mwonekano wa hadhi yangu, alikuwa ni kijana mzuri sema shida pengine ndo ziliukumbatia uzuri na utanashati wake na kumuachia muonekano wa kizee wenye kutoa taswira halisi ya kazi yake na muonekano wake, nilianza kumpenda Frank kwa jinsi alivyonifariji na kunifanya nisahau machungu niliyopewa na mchumba wangu, ni Frank ndiye aliyekuwa na mimi mda wote na kunifanya nione kila kitu kama ni kawaida, mara zote aliponiambia kuwa nisilie sana pengine mungu amenipangia mtu mwema ajaye atakaye nijali na kunifariji siku zote za maisha yangu basi moyoni nilikuwa nasema natamani angekuwa yeye. Ni mwanaume ambaye kwa kumsikiliza anayoyaongea na jinsi anavyopangilia yale atakayo kusema au jinsi anavyochambua mambo yake utajua kabisa ni kichwa.



    “Beatrice” aliita tena na sasa nilimuitikia.

    “unasemaje” nilimuitikia na wakati wote huu bado alikuwa pale chini ya ulinzi mkali wa polisi wa pale uwanja wa ndege.

    “kwanini unanifanyia hivi?” aliuliza na sikutaka kumjibu, nilijua nikimsikiliza nitamuonea huruma, niliamua kuondoka lakini nikiwa kama hatua kumi mbele nilimsikia tena akinisemesha nikasimama.

    “hukusoma barua niliyokutumia??” aliniuliza kwa sauti ya upole, kiukweli sikuwahi kuona barua yake na sikuwa na la kumjibu niliendelea kuondoka kuelekea upande wa pili wa pale uwanjani ili kuchukua gari langu.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “ile barua ilikuwa inaeleza kila kitu,,kaisome ili ujiepushe na dhambi hii unayoifanya kwasasa, kasome ile barua tafadhali,,nenda kaisome usiipuuzie” alizidi kupaza sauti huku akilia, niliendelea kutembea huku nikijiuliza barua gani anayoongelea lakini sikujali kitu nilikwenda mpaka nilipopaki gari yangu na wakati nageuza gari niliona baba yangu akiingia pale na Cadillac nyeusi na niliweza kuitambua na kumuwashia taa kisha alinifata nyuma na wote tulielekea mpaka kule Frank alipokuwepo.

    Vijana wanne walimshika na kumuingiza ndani ya gari kisha tuliwapa wale askari dola 1400 kila mmoja na walikaa kimya kisha tuliondoka pale uwanjani. Tulitembea kwa mwendo wa dakika kumi kisha tulikamata njia ya Lalana Dok na kuelekea Victoria Planete iliyopo upande wa kusini mwa pale uwanja wa ndege,,kama mwendo wa dakika 20 tulishuka na sasa tuliingia kwenye gari nyingine nyeusi aina ya hiace na sasa tulizidi kutokomea ambapo hata mimi sikupajua, kilomita moja mbele tulipita Vision Valley School na kuingia njia ya vumbi kisha tulikwenda mpaka hospitali ya Lutherani ya Ambohibao na hapo tulisimama kisha mzee alishuka na kuingia kule hospitali na baada ya dakika tano nilimoana akitoka nje na mzungu mmoja aliyekuwa amebeba begi, walisogea mpaka tulipokuwa na kuingia kwenye gari kisha tulianza tena safari , usiku ulikuwa umeshaingia na kama nusu saa niliona bango kubwa lililokuwa limeandikwa Futura Park nikagundua tulikuwa Andranomena, tulifika pale getini tukafunguliwa na kuingia ndani ya mbuga, hofu ilianza kunijia na mimi juu ya kilichokuwa kinaenda kutokea, tulienda mpaka tukatokomea kwenye pori na huko tulikuta nyumba yenye geti kubwa na tulifunguliwa.



    Tulipofika ndani Frank alitolewa kwenye gari na kupelekwa mpaka pale sebuleni kisha mimi niliambiwa nitoke nje, nilitoka nje na kuchungulia kwa pale dirishani, wakati huo Frank alikuwa ameshakaukiwa sauti, walimvua nguo zote na kumfunga kamba kisha walimning’iniza juu, nikiwa pale bado nikiendelea kuchungulia kilichokuwa kikiendelea niliona yule mzungu akimfata huku ameshikilia dawa ya kupuliza aina ya GV na wembe mdogo unaotumika mahospitalini kwenye upasuaji;

    “unamjuaje Mzee Ripson Odiego” aliulizwa swali la kwanza, na kwa mbali nilimsikia akijibu kuwa hamfahamu, baada ya kujibu vile wembe ule ulipitishwa kifuani kwake na kunifanya nisikie kutapika, damu zilianza kumtoka na kelele zilizidi pale walipompulizia ile dawa, nilianza kumuonea huruma na kuzidi kulia kichinichini nilikiwa pale nje, nilitoka mpaka mbele kidogo palipokuwa na bomba la maji nikaketi chini na kufungua maji kisha nilinawa uso wangu, sikujua kwanini nilimuonea Frank huruma wakati mimi ndiye niliyeenda kumkamata kule uwanja wa ndege baada ya kupewa taarifa na rafiki yangu kuwa amemwona mfanyakazi wetu pale uwanja wa ndege.

    Baada ya kupumzika kwa dakika tatu nilirudi tena kuchungulia pale, nikaona tena wakimsogelea huku yule mzungu akiwa amevaa ‘gloves’ mikononi.

    “Ulitumwa kufanya nini nyumbani kwa huyu mzee” aliulizwa.



    “nilikuja kutafuta kazi pale,, mimi ni mtanzania nilikimbia nchini kwangu baada ya….” Kabla hajamaliza kusema chochote alipitishiwa wembe tena na kupuliziwa ile dawa, nilizidi kulia kila alipolia lakini nilichohitaji ni ukweli tu auseme ambao hata hivyo hakuwa tayari kusema kabisa, kila mara alisisitiza kuwa yeye ni mtu mwema lakini hakuna aliyemsikiliza, baada ya kuulizwa kwa muda mrefu bila kujibu, yule jamaa alichukua kisu na kumuuliza swali tena kuwa ni taarifa gani alizifata nyumbani kwetu lakini alizidi kujitetea na kuomba apewe muda wa kujieleza,,hiyo haikumpendeza yule mtesaji na kumfanya amchome kisu kwenye paja, kisha alianza kumuuliza maswali huku akimkata kama vile alikuwa anakata mkate,,Frank alilia na mimi uvumilivu wa kuangalia akiteseka ulikuwa umekaribia kufika mwisho, zoezi hili halikufanikiwa kwani Frank aliendelea kusema kuwa yeye sio huyo wanaomtafuta, yule jamaa alirudi nyuma na kuangalia tena kisu kingine kidogo na aliporudi alimuuliza tena swali lilelile lakini majibu yalibaki kuwa yaleyale na hapo alishika uume wa Frank ka kutaka kuukata nilipiga kelele pale nje na kufungua ule mlango kwa haraka kisha niliingia ndani;

    “Inatosha, angekuwa ni mtu mbaya angesema ukweli baada ya mateso yote haya, muacheni jamani” niliongea huku nikizidi kulia, nilimfata baba yangu na kumpigia magoti wamuache kwakuwa pengine asemayo Frank ni kweli. Walimshusha na kumvalisha zile nguo, Frank bado alikuwa pale chini akilia na hali yake ilikuwa mbaya sana kwakuwa alikuwa akitetemeka, nilisikia tena kwa mbali akiniita na mimi nilimfata pale;

    “unasemaje Frank, unasemaje mpenzi” nilijikuta nikianza kumuita mpenzi na sikujua ilikuwaje lakini kwa hayo machache nilianza kumuamini.

    “nenda kasome ile barua” aliniambia kwa sauti ya chini sana.

    “barua gani?” nilizidi kumuuliza huku nikilia, sikujua ni barua gani anayoizungumzia.

    “barua uliyoletewa na yule binti wiki chache zilizopita, nenda kasome” bado maneno yake yalinichanganya na sikujua anazungumzia nini.

    ****

    Tulikuwa tumeshakubaliana kumpeleka Frank hospitali ili akatibiwe majeraha yote yaliyokuwa yamempata, yule mzungu alikusanya vitu vyake na kwenda kuviweka kwenye gari, kisha alirudi pale ndani, nilisikia akimwambia kijana wake asafishe lakini kabla sijaelewa maneno yale yalimaanisha nini, baba alinifata pale na kuniambia;

    “mwanangu wema huzaa dhambi, ukimpiga nyoka ukamkosa basi huwa na hasira sana, na akirudi huwa hatari kuliko mwanzo na hazuiliki” alinisemesha huku akiniangalia usoni

    “unamaana gari” nilimuuliza lakini alinigeuza uso kule alikokuwa Frank.

    “Muage” aliniambia maneno hayo na hapo niliona yule kijana akikoki bastola yake na kuachia risasi iliyopenya kwenye kichwa chake.

    “Nooooooo” nilipaza sauti hapo NILISHTUKA. Niliangalia huku na huku sikuona mtu yoyote nilipotazama nje niliona jua likichomoza kwa mbali huku ndege wakipiga kelele kuashiria ujio wa siku mpya, nilisikia mlango wangu ukigongwa na hapo ndipo niligundua kuwa NILIKUWA NAOTA.

    ****

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Nilinyanyuka na kuanza kutafakari yale niliyoyaota na hapo nilikumbuka juu ya ile barua aliyokuwa akiniambia ndotoni, nilienda kuoga na nilipotoka baada ya kunywa chai kazi ilikuwa ni moja tu, kutafuta ile barua, nilipangua vitu vyangu vyote lakini haikuonekana, nilikumbuka kuna siku iyo niliweka bahasha ile kwenye mkoba wangu niliouacha kwakina Lucrecia rafiki yangu aliyekuwa akiishi Anktaso, nilitoka nje nikakutana na baba, nilisalimia kisha nikaingia kwenye gari;

    “unaelekea wapi na mbona umevaa hivyo” aliniuliza wakati nikigeuza gari.

    “naenda Anktaso” nilimjibu kwa kifupi.

    “kuna nini” aliuliza tena,,maswali yake niliona kama yalikuwa yakinichelewesha.

    “kuna mkoba wangu niliuacha kwa Lucrecia ndo nataka nikaufate, kuna kitu muhimu ndani yake nataka nikisome” nilimueleza hayo na kisha aliingiza mkono mfukoni na kutoa fedha kisha alinipatia bila kusema ni za nini, nilipokea na kuanza safari ya kuelekea Anktaso, lakini baada ya mwendo wa kama dakika 15 nilikuwa nimefika Rabary, niliona gari ya Lucrecia ikiwa imeegeshwa sehemu, nilikwenda mpaka pale alipoegesha gari yake kisha nilishuka na kutazama ndani lakini sikuona mtu, nilisubiri kama dakika moja hivi na yeye alitokea;

    “mambo Lucrecia” nilimsalimu huku nikimkumbatia.

    “salama, unaenda wapi mbona mapema sana” aliniuliza huku akinishika nywele zangu.

    “nilikuwa nakuja kwako kuchukua mkoba wangu” nilimjibu kiuchovu.

    “mh!ndo uje asubuhi hivi?” aliniuliza tena.

    Nilimuhadithia Lucrecia kila kitu nilichokiota usiku ule, na baada ya hapo wote tuliondoka kuelekea kwao, nikiwa kwenye gari mda wote nilikuwa nikiwaza ni nini kimeandikwa kwenye hiyo barua, niliwaza sana juu ya ile ndoto lakini sikupata jibu ila kila nilipomuwaza Frank nilihisi mwili wangu unaishiwa nguvu.

    Tulifika nyumani kwa kina Lucrecia na nilichukua mkoba wangu na kuufungua lakini sikubahatika kuona ile barua, nakumbuka kabisa nilipewa ile barua lakini sikumbuki nilipoiweka. Akili yangu ilivurugika na hapohapo sikukaa sana niliamua kuondoka, njia nzima nilikuwa nikiipekua akili yangu kujua ni wapi niliweka ile bahasha lakini sikukumbuka kitu, machozi yalikuwa yananitoka mfulululizo kila nilipoikumbuka ile ndoto.

    “ninampenda Frank?” nilijiuliza moyoni lakini sikuwa na la kujijibu, hisia zangu zilikuwa dhahiri, lakini nilikuwa nimeshachelewa kwakuwa Frank alikuwa amefariki tena mimi nikiwa mmoja wa watu waliosababisha kifo chake.

    Nilifika nyumbani na kuanza kutoa tena vitu vyangu kimoja baada ya kingine, nilitoa kila kitu na kuvirudisha lakini sikuona kitu, nilikaa pale chumbani kama kichaa nikilia.

    “unalia nini” nilishtuka na kufuta machozi haraka, kisha niligeuka kuangalia ni nani nikakuta ni baba.

    “jana nimeota ndoto mbaya” nilimueleza hivyo tu nikawa kama ndo nimemualika pale chumbani, aliingia na kuketi kisha alianza kunihoji.



    “umeota nini binti yangu” aliuliza na mimi nilimuhadithia kila kitu lakini kabla sijamaliza kuhadithia nilikumbuka mahali ambapo ile barua inaweza kuwepo, nilitoka pale na kukimbia mpaka nje na kwenda kwenye lile ndoo lakuwekea takataka, lakini bahati mbaya sikukuta kitu, nilimfata dada wa kazi pale nyumbani na yeye aliniambia gari lakubeba takataka lilipita pale na kubeba uchafu wote asubuhi ya leo. Niliwasha gari na kuondoka pale mpaka kwenye jaa kuu la taka lililokuwa mjini, nilipofika pale ndo walikuwa wanajiandaa kuchoma takataka zote, niliwaomba nitazame kitu muhimu kilichokuwa kwenye zile takataka pale lakini hawakuniruhusu, walimwagia mafuta na zile takataka zilianza kuwaka moto kwa kasi kisha wao waliondoka,,nilitoka pale na kuingia mtaani kisha niliwaita vijana niliowaahidi nitawalipa na hasa nilipowatajia mimi ni mtoto wa nani walikuwa tayari kunifanyia kazi yangu, tulifika mpaka pale jalalani na kuanza kuuzima ule moto kisha kuanza kupekua kila sehem na hapo nilibahatika kuiona ile bahasha. Niliwapakia wale vijana mpaka kwenye benki iliyokuwa pale karibu a kutoa fedha kisha niliwapa na tukaachana,,niliendesha haraka na nilipofika nyumbani nilianza kuisoma ile barua kwa undani,,machozi yalinitoka kila nilipoisoma mstari kwa mstari, barua yenyewe ilisomeka hivi;



    Mpendwa Beatrice,

    Natangulisha shukrani zangu kwako kwa mema na faraja ulizonipatia kwakipindi chote nikiwa naishi hapo kwenu, ulikuwa msaada mkubwa sana kwangu kwakuwa nilipokuwa na huzuni wewe ulikuwa furaha yangu, nilikupenda na kukuheshimu si kama mtoto wa bosi wangu bali nilikupenda na kukuheshimu kama ndugu yangu. Mengi yametokea na yametokea kwa haraka sana, wewe ni mwanasheria tambua katika maisha yako hakuna haki kubwa kwa unayemtuhumu kama haki ya kumsikiliza. Kama ungenipa haki ya kunisikiliza leo hii usingejisikia mwenye hatia. Mimi si mpelelezi wala mimi si mtu wa aina uliyodhani, ningekuwa na ujasiri wa kuja tena kwenu leo ningekuomba unitazame machoni kisha uniambie kama naweza kuwa mtu mwenye nia mbaya na familia yenu. Nenda chumba nilichokuwa nalala mimi tazama nyuma ya kabati utaona ‘flash’ ifungue utakuta hadithi ndefu inayoitwa THE LOST PROFESSION hiyo ndiyo historia ya maisha yangu mpaka nilipofika hapo kwenu. Beatrice kwangu wewe ulikuwa wa thamani kubwa sana na mpaka leo nakupenda na kukuthamini licha ya yote yaliyotokea, naelewa kuwa hukufahamu ndio mana na pengine kama ungejua basi usingekubali hayo yanitokee mimi, maisha yangu yamekuwa magumu toka zamani, sikuwahi kupata ahueni ya maisha toka nimalize masomo yangu nchini Tanzania, lakini baada ya kufika kwenu nilihisi huo ulikuwa mwanzo mpya japo haikuwa hivyo. Sijutii kukufahamu wala baba yako, wewe kwangu bado nakupa uzito uleule kama mwanzo. Zingatia masomo yako, kuwa makini katika maisha, mimi sikufa, msamaria mwema aliyeniokota kule msituni alinisaidia na nimebahatika kusihi tena, lakini nategemea kuondoka kwenda Tanzania wiki moja ijayo, nimeona ni bora nirudi nikafie huko kuliko kufia ugenini, umasikini wangu umekuwa shida sana kwa uhai wangu. Mikono ya matajiri imeninyang’anya utu wangu na dhuluma yao imeukaba uhai wangu, niko tayari kufa ili nikapumzike na familia yangu huko waliko, siko tayari tena kuishi kama mkimbizi, narudi nyumbani Beatrice. Usijute ila jifunze, mimi nimekusamehe kwa moyo mmoja na sasa hata nikifa, hicho kitabu kitakuwa ni zawadi yangu kwako. Msalimie sana mzee mwambie mimi nimemsamehe, ila yale mateso mliyonipa yaishie kwangu, msimfanyie mtu mwingine kwakuwa si mazuri hata kidogo.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kwaheri Beatrice, nakutakia kila lenye heri katika maisha yako, soma sana na umtegemee mungu.

    Ni mimi Fisherman.



    Nilimaliza kuisoma hii barua na kugundua kuwa blauzi niliyokuwa nimevaa ilikuwa imelowa kwa machozi,kamasi na jasho.

    Nilinyanyuka haraka na kwenda kuangalia kwenye ile kabati nikakuta ile flash, niliwasha ngamizi yangu na kuichomeka kisha nilifanikiwa kuiona ile hadithi, niliisoma kwa muda wa masaa miwili na nusu na nilikuwa nimemaliza, nililia sana na hapo nilimfata baba nakumpa ile barua na ile hadith asome, wote tulijuta lakini hatukuwa na la kufanya.

    “baba nataka nimfate Fisherman huko aliko, naamini atapatwa na jambo baya” nilimuambia mzee wangu lakini alikataa kabisa kusikia jambo hilo,,nililia usiku na mchana lakini hakukubali, niliandika kisirisiri barua ya kuahirisha mwaka mzima wa chuo na niliruhusiwa, nilirudi na kumtishia baba kuwa ningejiua kama asingeniruhusu na yeye ikabidi akubali. Nilisoma katika ile hadithi maeneo matatu ya Tandale,Kimara na Kibaha, niliingia kwenye ‘google map’ nikachukua ramani izo, baba alinisaidia kuwasiliana na rafiki yake ambaye alikuwepo nchini Kenya na huyo rafiki yake alisema anamtoto wake wa kike ambaye yuko Tanzania hivyo angenipokea na ningekaa kwake.



    BAADA YA WIKI.

    Asubuhi na mapema nilikuwa nimeshafika Ivato International airport kwaajili ya safari yangu ya kwenda nchini Tanzania kumfata Fisherman, nilikuwa sielewi ningempataje hasa ukizingatia kuwa ilikuwa ni nchi kubwa lakini nilikuwa na uhakika wa kumpata,,Saa 12:00 kwa saa za Madagascar ndege ya British airways iliondoka uwanja wa ndege na kuanza kushika anga tayari kwa safari ya kuelekea Misri na baadaye Afrika ya kusini kisha Tungepanda ndege ya shirika la Emirates kwa kuelekea Tanzania.



    “Maisha ni kuishi, lakini maisha ni vile siku yako inavyoisha. Uzito wa jambo hutegemea na mapokeo halisi ya yule afikwae na jambo, utumwa wa akili zetu husababishwa na mapokeo mpauko ya uhalisia wa mambo. Uhuru wa fikra usio na kikomo huleta utumwa wa nafsi. Kila mtu anaweza kuwa vile atakavyo ila tunapishana namna na jinsi ya utekelezaji wa yale tuyaaminiyo. WEWE NI BORA ZAIDI ILA UBORA WAKO HUISHIA PALE WA MWENZAKO







    “All passangers we are about to land in Tanzania, the British Airways Corporation is hereby wishing you a all the best in Tanzania and thanks for choosing us”(Abiria wote tunakaribia kutua Tanzania, shirika la ndege la Uingereza linakutakia mafanikio mema ukiwa Tanzania na asante kwa kutuchagua), ilikuwa sauti iliyonishtua toka usingizini na nilipotazama nje niliona mataa kwa mbali, nikagundua lilikuwa ni jiji la Dar es Salaam, kwangu hapa nilikuwa napaita uwanja wa mateso na kwasasa nilikuwa nimekuja kujaribu kete yangu ya mwisho kabla ya kifo changu, niliamini kabisa kuwa hakukuwa na jipya tena kwenye maisha yangu lakini sikujali kwakuwa sikuwa na cha kupoteza tena hapa duniani, watu wote muhimu walishaondoka kwenye maisha yangu, na sasa mtu pekee aliyekuwa muhimu kwangu alikuwa Natasha ambaye hata hivyo sina mategemeo ya kuwa na yeye tena, nilikuwa nampenda sana lakini hiyo haikuwa sababu ya mimi kumtafuta ili kumwambia ukweli wowote, hiyo haikuwa sababu ya mimi kuhatarisha tena maisha yangu kwa ajili yake. Maneno aliyoniambia baba yake na Natasha siku ile alipokuja pale nilipokuwa nikiishi yaliendelea kuwa na maana kubwa sana katika maisha yangu, aliniambia PESA ITAOA PESA, akimaanisha kuwa sina hadhi ya kumuoa mwanae kwakuwa mimi nilikuwa masikini, sikukataa hilo lakini niliamini mapenzi niliyokuwa nayo kwa Natasha yalikuwa ni zaidi ya utajiri, niliamini kama ningepewa uhuru na haki ya kumiliki elimu niliyokuwa nayo basi leo hii ningekuwa mtu mwenye uwezo kiasi cha kuwa na hadhi ya kumuoa Natasha.



    Natasha hakujali umasikini wangu, yeye alijali mapenzi ya kweli niliyompatia, hakuwa na shida ya hadhi kwakuwa alikuwa tayari anahadhi. Kama hata angekuwa ni mtoto wa masikini muuza gongo lakini uzuri wake wa asili ungebaki kuwa thamani na hadhi kubwa iliyosubiri marashi ya upendo, hadhi na ushawishi wa pesa katika mapenzi yalikuwa ni mambo ya zamani ya koo za kifalme au zile za kichifu, lakini kwa mfumo wa dunia ya sasa pesa haiwezi kuwa ndiyo kipimo cha mapenzi ya kweli hata kidogo, kama mzee Rweikaza angegundua ni kwa kiasi gani mwanae anahitaji faraja ya kweli basi asingeruhusu fikra potofu zilete kilema cha ufikiri kwenye akili yake na kuamua kunipoteza kimalengo na kimaisha kabisa na sasa nilikuwa kama mpuuzi yeyote yule aliye na lakusema asilokuwa na ushahidi nalo. Leo hii katika jamii sikuwa kitu sio tu kwasababu nilidhulumiwa haki yangu, hapana ni kwakuwa sasa sina namna ya kufikia pale nilipoamini pengine ningefika kwa jitahada za mwanzo nilizozifanya. Sikuwa na cha kujifunza zaidi kwakuwa darasa nililopewa kwa upendo wangu mwenyewe ni mateso tosha. Kilichoniumiza akili ni kivipi mwanasiasa aukatae umasikini kupiga hodi kwenye nyumba yake ilihali anahubiri kuwa pamoja na wananchi,,ama kweli mwenye pesa si mwenzake, nilipiga moyo konde na kusonga mbele, muhimu ni pumzi kwanza.



    *****



    Nilikuwa nimeshashuka toka kwenye ndege na sasa nilikuwa uwanja wa ndege wa Mw. JK Nyerere, ni miaka zaidi ya mitano toka nimeondolewa na wenye mabavu katika nchi yangu, niliyohangaika kuuimba Tanzania Tanzania nakupenda kwa moyo wote kipindi nikiwa shuleni, baada yakutoka nje kabisa ya pale uwanjani niliitazama tena sehemu ile na kukumbuka siku niliyoshuka kutoka Pritoria nikiwa na shahada ya pili ya sheria na kupokelewa na Natasha;

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Frank sasa kusoma tena basi mpenzi wangu, utakuja kuzeeka nisikufaidi, elimu uliyonayo kwasasa inatutosha kabisa kuanzisha maisha yetu na tukaishi vizuri, sasa hivi ukajishikize kwanza kwenye Kampuni Fulani ya wanasheria nimeshaongea nao, alaf baada ya muda Fulani kuna nafasi zitatoka za kwa mwanasheria mkuu wa serikali nitakuunganisha huko moja kwa moja alaf baada kama ya mwaka utaingia UN” nakumbuka maneno haya aliniambia tulipokuwa katika chakula cha jioni pale Zanzibar Retreat Hotel kwenye kisiwa cha karafuu, hii ilikuwa ni siku ya pili toka nitoke Chuoni, nakumbuka tulikaa Zanzibar siku mbili tukila raha na Natasha, sikuwahi kufikiri kama yangekuja kunifika yaliyotokea na kama ningejua basi pengine ningemwambia tutoroke kabla halijajiri lolote, lakini ndio hivyo tena, sisi wote tulikuwa vipofu wa linalotokea mbele yetu. Nakumbuka tukiwa Zanzibar niligusia swala la mimi na yeye kushindwa kutimiza malengo yetu kutokana na utofauti wa kiuwezo kati yangu mimi na familia yake lakni kwake halikuwa tatizo,



    ITAENDELEA

    0 comments:

    Post a Comment

    Blog