Search This Blog

Thursday 29 December 2022

C.O.D.EX 4 (A MISSING SOLDIER) - 4

 

  Simulizi : C.o.d.ex 4 (A Missing Soldier)

Sehemu Ya Nne (4)


Ndani ya nchi ya Marekani, gari la polisi alilokuwa analiendesha Idris, lilikuwa linachoma mafuta yake kuelekea katika Jiji la New York ambalo lilisifika kwa kuwa ulinzi mkali, labda kuliko jiji lingine pale Marekani. Lilikuwa na ulinzi huo kwa sababu ya biashara kubwa nyingi kufanyika eneo hilo pamoja na kubarikiwa watu maarufu duniani. Lakini hiyo, haikuwa sababu ya Idris kuacha kuchoma mafuta ya gari alilokwapua. Aliendelea kubadilisha gia kila alipokuwa anapata nafasi ya kufanya hivyo. Gari lilikuwa linakwenda kwa mwendo wa kasi kupita maelezo.


Asubuhi na mapema, jua linachomoza, bado gari la wababe wale lilikuwa halijafika katika Jiji la New York na mara kwa mara walitazama ramani ya kwenye gari lao ili kuona wamebakiza umbali gani kuweza kufika katika jiji hilo.


“Saa moja pekee, inaweza kutufikisha tunapotaka.” Idris aliongea na maneno hayo yalimuingia vema mwanadada Merice ambaye naye kuonesha alikuwa kadhamiria, aliikoki bunduki yake na Idris akazidi kuichakaza rami kwa kukanyaga mafuta.


Upande wa Uzo, alikuwa kasimama mbele ya wanajeshi watano ambao wao walikuwa ni wa aina tofauti na wale walio pita. Hawa walikuwa wamevaa nguo maalumu kutokana na kile wanachokifanya. Wanaitwa Pro. Soldiers ama kwa kirefu Professional Soldiers yaani kwa lugha rahisi, ni wale wanajeshi wenye taaluma binafsi.


Katika hao wanajeshi watano, mmoja alikuwa kavaa nguo za mpira wa miguu na alikamata mpira huo mikononi mwake. Mwingine yeye alikuwa kavaa nguo nyeupe na mkononi kakamata rungu pamoja na kitenesi kilichotengenezwa kwa marumaru, huku kichwani kwake akiwa kavali kofia kama ile ya pikipiki lakini mbele ikiwa na nyavu. Ukimuona katika mavazi hayo, utajua wazi anacheza mchezo maarufu huko India au Australia, wanauita Cricket.


Mwanajeshi mwingine, yeye alikuwa anamwili mkubwa na alivaa mavazi makubwa kama yeye. Alikuwa pia kavalia kofia kama ya pikipiki, lakini yeye alikuwa anampira wenye umbo kama la yai. Huyu alionekana wazi kuwa anacheza mchezo wa kutumia nguvu sana wa Rugby. Katika wanajeshi hao watano, pia kulikuwa na mwanadada mwenye nywele ndefu na alikamata kitenesi cha kawaida pamoja na fimbo moja ambayo ilikuwa ina nyavu kwa mbele. Ilikuwa ni fimbo maalumu kwa ajili ya kucheza mchezo wa Tennis. Na wa mwisho yeye alikuwa kavaa koti lenye rangirangi nyingi, na miguuni alivaa viatu ambavyo chini vilikuwa na matairi. Mkononi alikamata fimbo ya chuma ambayo kwa chini ilikuwa bapa. Na mwanajeshi huyu alikuwa anakirusha kitu fulani cha chuma ambacho kilikuwa cha duara lakini kipo kama kifuniko cha kopo la mafuta ya kupaka.


“Nimewaita hapa kwa kazi moja tu. Kazi ya kuua au kumleta mbwa mmoja akiwa hai.” Alianza kuongea Uzo baada ya kimya kifupi kilichotawala tangu wanajeshi wale waletwe na Simeria. “Ni mwanajeshi ambaye tayari amehangamiza baadhi ya wanajeshi wetu. Na nawatuma nyie kama chaguo langu la mwisho. Na najua, mtafanya kile ambacho nakiota.” Akaongeza. Wanajeshi wale ambao walionekana wana uchu wa kufanya kazi yao, walifarijika kwa maneno ya Uzo ambaye alizidi kuwajaza maneno yake. “Si mwanajeshi rahisi kama mnavyodhani, ila nina uhakika kuwa, atakuwa rahisi sana kama mkifanya kazi hii kama timu moja. Nyie ni wanamichezo, lakini mnacheza michezo tofauti. Mkiiweka michezo kwa pamoja, mnaweza kufanya makubwa sana.” Akaendelea kusifia kila anapopata nafasi ya kufanya hivyo. Na wale wanajeshi ambao walikuwa hawana tabasamu, waliendelea kusikiliza kila ambacho mkubwa wao alikisema.


“Tumekuelewa mkuu. Tunaanzia kazi wapi?” Akauliza mwanajeshi mmoja ambaye alikuwa anamwili mkubwa kuliko wenzake. Ni yule mcheza rugby.


“Wapo njiani wanakuja New York. Hivyo tutawaweka nyie mahali ambapo wataanza kuingilia. Tumewakataza polisi wote kuwazuia. Hii ni nzuri sana kwenu kwa sababu hamtaingiliwa na yeyote kwenye suala hili. Hivyo mkipata nafasi ya kuua hawa paka, ueni tu.” Akajibu Uzo.


“Wapo wangapi?” Akauliza mwanadada mcheza tennis.


“Wapo wawili. Na mmoja ni mwanamke lakini hana sumu kabisa. Ni huyu wa toleo la kwanza la C.O.D.EX. Ila huyu mmwanaume, hatujui katengenezwa kwa njia gani. Ndio maana tunamtaka sana yeye kuliko huyu mwanamama. Huyu wa kiume akija maiti au mzima, tutamchunguza ili tuwaunde wengi kama yeye. Anaonekana kaundwa kitaalamu sana.” Uzo alijibu na kuwasha video ambayo ilionyesha jinsi Idris anavyopambana na wale wanajeshi wengine huku akiwapiga mapigo ya kuzima na kuwaka. Yaani anajitokeza na akijitokeza, basi ni balaa.


“Yupo vema.” Mwanadada alisifu jinsi alivyoona ile video ya Idris anavyoweza kuwapiga na kuwagalaza vibaya wanajeshi wa Uzo.


“Lakini hawezi kuwa vema zaidi ya hii.” Mwanajeshi mwenye mwili mkubwa, ambaye alikuwa na taaluma ya kucheza mchezo wa kutumia nguvu, rugby, aliongea huku na kuukamata mpira wake wa rugby na kuubonyeza hadi kuupasua.


“Safi sana jemedari,” Uzo alisifia kitendo cha mwanajeshi mcheza rugby na kisha kwenda hadi kwenye kabati moja lililokuwa limefungwa kwa namba maalumu na kubonyeza namba hizo. “Na ndio maana nimewaita hapa ili mfanye kile nachotaka,” Alizidi kuongea huku akibofya namba moja baada ya nyingine. Kisha akabonyeza ‘ok’ na kabati hilo likafunguka. “Na kwa sababu nataka mshinde vita, nimewatengenezea silaha maalumu kwa ajili ya kushinda vita hiyo.” Vifaa vya michezo vikaonekana ndani ya kabati hilo na kuwafanya wale wanajeshi kila mmoja aendee silaha yake kutokana na mchezo anaocheza.


“Hii ni kubwa kuliko tulivyotegemea bosi.” Mwanajeshi mmoja aliongea baada ya kuchukua mavazi na kuyavaa, kisha kukamata silaha inayomuhusu.


“Kila kitu kipo hapa kuhusu silaha hizo. Utazitumia kama unavyoweza kuzitumia ukiwa uwanjani au kwenye mchezo wako.” Sauti hiyo ilienda sambamba na Uzo kuwasha video ambayo ilitoa maelezo jinsi ya kutumia silaha hizo za kimichezo. Zilikuwa ni silaha hatari kuliko wanajeshi wale walivyotegemea. Na kila mmoja aliahidi kuzitumia kwa jinsi alivyoelekezwa. “Chochote ambacho kitakuwa kikwazo kwenu, kivurugeni. Iwe wananchi au wana usalama. No mercy.” Uzo alitamka hayo akimaanisha wanajeshi wale wasiwe na huruma katika kazi yao. “Nendeni kazini, kila kitu nitakiona kupitia hivyo mlivyovivaa. Na kumbukeni, mavazi mliyoyavaa, naweza kuyafanya yakawaongezea nguvu pale nitakapopaswa kufanya hivyo. Na ninaweza kuwaua kama mkionekana kuleta huruma au kutaka kusaliti.” Wanajeshi wote wakakubaliana na hilo bila kuonyesha tabasamu. “Tawanyikeni. Nendeni eneo la tukio.” Akatoa amri na wanajeshi wale walitoka ndani ya maabara hiyo kwa mstari.


Nje ya jengo la kutengenezea wanajeshi wa C.O.D.EX, walionekana wanajeshi wale wakipanda helikopta maalumu kwa ajili yao tayari kwa kwenda kupambana na Merice akiwa na Idris. Helkopta ilikuwa juu ya ghorofa refu ambalo lilijengwa pembeni kidogo mwa Jiji la New York. Baada ya wote kupanda, helikopta ikakata mawingu.


Idris aliliingiza New York gari alilochukua toka kwa polisi kwa kasi ya hatari kabisa na kusababisha kimuhe muhe na taflani ndani ya jiji lile. Kila mwananchi alishangaa kasi ya ajabu ambayo Idris aliingia nayo katikati ya jiji lile.


Akiwa katika kasi hiyo, alijikuta ghafla akikanyaga breki na macho yake kutazama mbele huku akiwa kayakodoa na kushindwa kufanya lolote zaidi ya kuacha injini ya gari lile kunguruma pekee.


“C.O.D.EX Proffesinals.”Alisikika Merice huku naye macho yake yakiwa yanawatazama wanamichezo watano waliyosimama katikati ya barabara kubwa ndani ya jiji lile kongwe.





“Mjinga kaamua kutuma jeshi lake la mwisho.” Idris aliongea huku macho yake yakimanika zaidi na wale wanajeshi. Kompyuta aliyopandikizwa kwenye kichwa chake, tayari ilikwisha wasoma wanajeshi wale na walionekana kuwa ndio jeshi la mwisho kuundwa na C.O.D.EX.


“Nilisikia hilo. Na mama ndiye aliwaunda hawa baada ya wale advanced. Ila hawa, ni hatari kwa sababu hufanya mazoezi kwa pamoja kutokana na michezo yao. Wana ubovu mmoja tu, ambao ukiudhibiti, unakuwa umewashinda.” Merice alitabainisha kidogo anachokijua.


“Ubovu wao ni nini?” Idris aliuliza na kuendelea. “Naona pia wamevaa mavazi kama silaha. Na kila kitu mwilini mwao ni silaha.”


“Ubovu wao ni huyo mcheza mpira wa miguu. Wao wamembatiza jina la Maradona. Ni hatari sana huyo. Ukimdhibiti, unakuwa umefanikiwa. Ila ni hadi uwadhibiti hawa wengine.” Merice akajibu bila kuongeza neno.


“Si mimi peke yangu wa kuwadhibiti hawa. Naamini kwa pamoja, tunaweza kwa kutumia silaha hizi za Agent Zero.” Idris aliongea na kukoki bunduki yake na kuchukua silaha zingine na kuziweka kwenye mavazi yake tayari kwa mapambano. Naye Merice hakuwa nyuma kufanya vile mwenzake alivyofanya.


Raia wengi walisimama pembeni wakiwashangaa wale wanajeshi jinsi walivyojipanga kwa kuvutia mbele ya gari la Idris. Waliyoweza kuwapiga picha, walifanya hivyo, na waliyoweza kuwachukua video, pia walibahatika kufanya hivyo. Lakini zaidi, ilikuwa ni hatari kubwa sana kwao.


Maghorofa marefu yaliyotapakaa katikati ya jiji lile, yaliendelea kuonesha matangazo ambayo yaliwekwa kwenye runinga kubwa za maghorofa hayo. Wananchi waliendelea kutizama kile ambacho kinataka kutokea katikati ya jiji la New York.


Dakika tano mbele, Idris alichomoza toka kwenye mlango wa gari alilolichukua. Na upande mwingine, Merice naye alichomoza huku akiwa kakamata vema mtutu wake tayari kwa mapambano ya kivita ambayo hayakuwa na jina.


Raia waoga walianza kujikusanya wao pamoja na watoto wao, na kukimbia mbali kabisa na eneo lile ili kunusuru roho walizopendelewa na MUNGU.


“Muda wa Vita vya Tatu vya Dunia. Ni vita kati ya mashine na mashine. Ni vita kati ya vilivyoumbwa na binadamu mwenyewe, na vile vya MUNGU.” Uzo aliongea akiwa ofisini kwake akitizama vema tukio lililokuwa linaendelea kuchukua nafasi katikati ya New York.


Idris na Merice wakasogea mbele ya gari walilokuja nalo na kuweka mitutu yao ya bunduki sawia kuwaelekea wale wanajeshi wanamichezo.

Risasi kadhaa zikachomoka kwenye bunduki za Merice na Idris na kuzidisha mkimbizano mkubwa ndani ya jiji lile. Risasi hizo ziliwaelekea wale wanajeshi na wao wala hawakuwa na wasiwasi zaidi ya kupinda huku na huko na risasi hizo kupitiliza bila kuwadhuru. Walizikwepa vema sana bila miguu yao kuondoka pale waliposimama.


Idris na Merice walipoona hivyo, tayari akilini mwao walikwishajua kuwa watapoteza risasi nyingi sana kama watapambana kwa kusimama eneo moja. Mawazo hayo yalikatiza vichwani mwao haraka, na walipoamua kufanyia kazi mpango wa pili wa mapambano, ndipo hapo jiji la New York lilipoanza kuchafuka.

****

Katika Jiji lingine kabisa, mbali na New York na mpakani mwa Mexico, nazungumzia Jiji la Texas. Jiji ambalo linasifika kwa ufugaji wa farasi pamoja na kuwa na polisi wakongwe waitwao Rangers. Bwana mmoja aliyekuwa anaangalia runinga yake, alijikuta akitabasamu baada ya kushuhudia kile ambacho alikuwa anakitazama kwa muda mrefu kwenye ile runinga.


Bwana yule akainuka na kwenda hadi kwenye jokofu lake na kulifungua, kisha akatoa kinywaji kimoja kikali kilichokuwa kwenye chupa ndefu. Bila kumimina kwenye gilasi, akaanza kuigida vivyo hivyo kwenye chupa yake.

Baada ya kuridhika, akairudisha chupa ile kwenye jokofu na kabla hajafunga jokofu lake, akapekua nyuma ya chupa kadhaa. Huko nyuma ya chupa hizo, akakukatana na kidubuwasha kimoja ambacho kimetuna kwa mbele na kina rangi nyekundu. Akakibofya, nacho kikaingia kwa ndani na hapohapo, mlango mkubwa wa ukuta uliokuwa nyuma ya jokofu, ukaanza kufunguka.


Baada ya kumalizika kufunguka, bwana yule ambaye alikuwa ana asili ya Kiafrika, na kavalia jinzi nyeusi pamoja na fulana nyekundu iliyombana sana, aliingia kwenye chumba kile kilichokuwa nyuma ya jokofu. Na mlango wa ukuta ulijifunga ukimuacha jamaa akiwa ndani yake akiangaza huku na huko.


“Muda wa kazi umewadia.” Alijisemea jamaa yule na kishja akaenda kwenye meza kubwa ya kioo na kubonyeza namba fulani, na kioo kile kikajitoa rangi nyeusi (tinted) iliyokuwa inaziba usione kilichokuwa ndani. Na baada ya kujitoa rangi ile, kioo kile kilijifungua na zikaonekana silaha mpya na za kisasa za kivita.

Jamaa akashusha pumzi ndefu na kisha akaanza kuchagua silaha ambazo alizihitaji kwa ajili ya kazi ambayo hadi muda huo ilikuwa haijulikani ni kazi gani na anaenda kuifanyia wapi.


Silaha kadhaa zilikuwa zimechaguliwa na yule jamaa baada ya kufungua makabati mbalimbali ambayo yalikuwa yamezagaa ndani ya chumba kile kilichoonekana ni maalumu kwa ajili ya silaha.


“Haloo makao makuu.” Jamaa aliongea kwa simu baada ya kuchukua baadhi ya silaha na kuweka kwenye begi maalumu la kubebea. “Agent Unknown, 000 Unknown.” Akajitambulisha kodi zake na upande wa pili ukamuitikia. “Watahiniwa niliyokuwa nawasubiri, wamejitokeza leo hii huko New York.” Akawapa taarifa kwa kile alichokuwa anakifahamu.


“Na sisi tumewaona” Ikajibu sauti ya kike upande wa pili wa lugha ya Kiingereza. “Tayari tumemuagiza mia na tano kwenda kukusaidia kupandikiza chipu ya kuwafuatilia popote watakapokwenda.” Akaongeza mwanadada.


“Muhase asifanye lolote. Asiingilie ule ugomvi.” Agent Unknown, aliongea kwenye simu.


“Hilo analijua. Akipandikiza hiyo chipu, taarifa za wanapokwenda itakuja kwenye simu yako haraka.” Akajibu mwanadada na kutoa maelezo mengine mafupi.


“Vema. Safari hii lazima wateketee.” Akaomgea jamaa aliyejiita kwa kodi ya Agent Unknown.


“Nikuitakie kheri Agent. Ukimaliza kazi hii, nadhani utachukua likizo ya mwaka mzima.” Akaongea dada huyo maongezi mengine binafsi.


“Nitafanya hiivyo kwanza. Kisha nitakuja China kukuchukua mrembo.” Akatania Agent Unknown.


“Wewe, acha hayo maneno, bado upo hewani na maongezi yako yanarekodiwa.” Akaonya dada yule ambaye hata kama hujamuona, ni wazi alikuwa katabasamu kwa yale maneno.


“Tatizo nini sasa? Au vibaya kwa mtoto wa Kichina kuchukuliwa na mweusi kama mimi?” Agent akauliza na hakumpa nafasi ya kujibu yule mwanadada, akapandishia maongezi yale. “Au labda sina mvuto wa kuja kwenye familia yako na kujitambulisha kuwa mimi ndiye mwanaume wa pekee katika hii dunia, ambaye naweza kukulinda kwa lolote baya na kukupa kile ambacho wengi sa……” Hakumaliza kauli yake, akawa kakatishwa na sauti nzito.


“Acha ujinga Agent, nenda kazini. Kamalize hiyo misheni kisha njoo China kuchukua barua yako.” Simu ikakatwa baada ya maneno hayo ya kijeshi.


“Shit. Sasa nimefanyaje hadi akate simu yangu? Kwani kapiga yeye au mimi? Huyu bosi boya sana. Wakisema nimuue, nitamuua kwa sababu ya kunibania kumchukua mwanaye.” Akajiongelea mwenyewe Agent Unknown huku anatoka kwenye chumba kile na begi la silaha mkono wa kulia.


Akabonyeza namba kadhaa kwenye ukuta ule, na makabati yote yakajifunga na ukuta ule aliyoingilia, ukaanza kufunguka na kumpa nafasi ya yeye kutoka na moja kwa moja akaenda kwenye runinga ambayo alikuwa anaitazama kabla hajaenda kwenye kile chumba.


Hapo alimuona mwanajeshi mmoja mweusi pamoja na mwanadada (Idris na Merice) wakiwa wamezungukwa na wachezaji wa michezo mbalimbali na wachezaji wale wakiwa wanawavuta kwa nyaya nyembamba zilizojichimbia kwenye miiili yao. Hali ilikuwa tete kwa wale wanajeshi wawili na kituo kimoja cha habari nchini Marekani, kilikuwa kinaonesha tukio lile moja kwa moja kutoka Jiji la New York.

*****

Uso wa Idris ulikuwa unawatazama wale wanajeshi wa jeshi la CODEX kwa uchu wa ajabu na pale walipoanza kuwavamia, yeye pamoja na Merice, hali ikazidi kuwa mbaya sana hasa kwa raia wa kawaida ambao walikuwa bado wanahisi wanaangalia filamu ya kusisimua moja kwa moja kupitia macho yao.


Idris alikuwa anamimina risasi nyingi za kawaida bila kutumia zile alizotengenezewa na Agent Zero. Na risasi hizo wakati anazitema, alikuwa anasogea mbele kwa kasi huku anapishana pishana na Merice ambaye naye hakuwa nyuma kuwashambulia wale wanajeshi kwa silaha zake za kawaida.


Wanajeshi wenye taaluma, walikuwa kwenye kazi ya ziada kukwepa risasi za Idris na Merice na wakati huohuo, wakiwa makini pia kumuangalia Idris asipotee kimazingara na kuwatokea kwa nyuma. Hivyo walichofanya, ni kuseti nguo zao ziweze kuzuia risasi na vilevile, kuweka duara ambalo liliwasaidia kuona pande zote ambazo kama Idris atatoweka ghafla na kutokea upande mwingine, basi wangeweza kupambana naye. Lakini haikutokea hivyo bali Idris na Merice kufika hadi pale walipo na kuanza kupambana nao uso kwa uso bila silaha.


Bunduki iliyokwisha risasi, aliirusha kwa nguvu Idris kumuendea bwana mwenye mwili mkubwa na bunduki ile yule mcheza Rugby, aliikwepa na kwa haraka kabla hajageuka, Idris aklikuwa kafika na kumshushia ngumi nzito ya uso iliyompaisha hatua tano nyuma toka pale aliposimama. Wenzake wakiwa hawana hili wala lile kwa pigo lile la kushtukiza, walijikuta nao wakiambulia ngumi nyingi za haraka zilizowatupa umbali uleule ambao alitupwa mcheza Rugby.


“Mmeingia pabaya madogo, bora mngeenda kucheza michezo yenu huko porini na si kwangu.” Idris aliongea wakati wale mabwana wakiwa chini wanajizoa zoa ili kunyanyuka.


“Hapana Soldier, wewe ndiye umekosea kuja mjini.” Aliongea mcheza mpira au Maradona na saa hiyohiyo akachanganya mikono yake, mpira wa miguu ukatokea na kuuweka chini kisha akaupiga shuti zito sana. Idris aliuona jinsi unavyokuja na kwa mkono wake mmoja akaudaka mpira ule. Lakini kabla hajafanya maamuzi, mcheza mpira wa miguu alibofya rimoti yake na mpira ukalipuka na kumrusha vibaya Idris bila kutegemea huku mkono wake ukiwa unawaka moto sababu ya mlipuko.


Merice kuona hivyo, akaanza kumkimbilia Iris lakini mwanajeshi mwenye viatu vya matairi, alichomoka kwa kasi akisaidiwa na viatu vyake na huku kakamata fimbo ya mchezo wake, akamfikia Merice na kumchapa ngwara nzito kwa kutumia fimbo ile.


Wakati huo Idris alikuwa anajaribu kujiinua pale kwa mkono mmoja, ndipo alishuhudia kichapo kizito kikimkuta mshirika wake Merice.


“Yaaah.” Idris alilia kwa uchungu na kusimama wima kisha akawaangalia wale wanajeshi wakiwa wamejitayarisha kupambana naye na kabla hajafanya lolote, alishuhudia mpira wa Rugby ukimuijia. Akawaza nao kuwa akiudaka, basi utalipuka hivyo aliamua kutaka kuukwepa. Lakini kabla haujamfikia, mpira ule ulilipuka na kutoa sindano nyingi sana ndogo ndogo zilizomchoma kila mahali kwenye mwili wake.


Na wakati akiwa katika kimuhemuhe hicho cha kujiokoa kwenye zile sindano, kishindo kikubwa cha kukimbia, kilisikika mbele yake. Alipoangalia, alikuwa ni mwanajeshi mcheza Rugby ambaye alimkumba kwa bega lake sehemu ya kiunoni na kumtupa Idris mbali kama mzigo. Japo Idris si mtu wa kuhisi maumivu, lakini baada ya kudondoka, zile sindano zikazidi kujikita ndani ya mwili wake, na uchungu ulimuingia kwa sababu sindano zile zilikuwa na sumu maalumu ya kumnyonya nguvu zake.




Kijana yule mwenye asili ya weusi, ambaye alichukua uraia wa Tanzania na ambaye aliumbwa tena baada ya kufa, akawa mwanajeshi mwenye kemikali hatari za C.O.D.EX, aligalagala pale chini kwa sababu ya zile sindano zilizotoka kwenye mpira wa rugby. Wakati huo naye Merice alikuwa yupo chini kakamatika vema na yule mcheza mchezo wa fimbo. Mwenye viatu vya matairi.


Idris baada ya kugaa gaa pale chini, aliamua kulala chali, akawa analitazama anga ambalo halikuwa na jua kali, na wala jua hilo halikuwa katikati ya dunia kwa muda ule.


“Idris fanya kitu.” Aliisikia sauti ya Merice kwa mbali ikiongea maneno hayo. Macho ya Idris yakaingiwa na mwanga fulani machoni mwake, picha za mwanamke akimtakia heri ya siku ya kuzaliwa, ikamuijia. Na picha za bwana mmoja wa makamo aliyekamata keki ya siku hiyo ya kuzaliwa, nayo ilimuijia huku sura za watu wengi wakimuimbia kijana mdogo wimbo wa siku ya kuzaliwa.


“Happy Birthday mwanangu.” Mwanamke aliyekuwa pembeni ya kijana yule mdogo, ilimuingia masikioni vema. Mtoto yule alitabasamu na mama yake akamkumbatia na wakati huo keki ilitua mezani na bwana aliyeileta, naye alimuita mtoto yule mwanangu.


Mishumaa saba juu ya keki ile ilizimwa na mtoto. Keki ilianza kukatwa tayari kwa mtoto yule kuwalisha watu wachache waliyoalikwa kwenye tafrija ile ndogo. Wakati tendo lile linaendelea, mara aliingia bwana mwingine mwenye suti nyeusi na kutoa samahani kwa kuchelewa kwenye sherehe ile. Wote walimuelewa na moja kwa moja bwana yule alimuendea mtoto yule,


“Happ Birthday, Best.” Alimtakia heri ya kuzaliwa na kumkabidhi kibox kidogo kilichofungwa na karatasi la zawadi. Mtoto yule akatabasamu na kumkumbatia yule bwana.


“Ahsante Dokta Ice.” Mtoto Best alimshukuru yule bwana aliyemkabidhi kiox kidogo cha zawadi. Alikuwa ni Dokta Ice, baba wa Merice na mume wa zamani wa Simeria. Alikuja kwenye tafrija ndogo ya familia ya Dokta Bouncher ambaye ni mwanzake waliyeunda upya kanuni (formula) ya C.O.D.EX.


“Happy Birthday Best.” Mtoto mdogo wa kike naye alimpa saa ya mkononi Best huku anamtakia heri ya kuzaliwa. Dokta Ice akamnyanyua mtoto yule wa kike na kumbusu kwa upendo.


“Na wewe yako ikifika, atakuja kukuletea gari, sawa Merice eeh.” Dokta Ice alimuambia binti yake na mtoto yule alicheka kwa furaha na kumkumbatia zaidi baba yake.


Baada ya dakika kadhaa, Dokta Ice na Dokta Boucher, walitoka nje na kuanza kuongea peke yao. Nyumba ambayo alikuwa anaishi Best na familia yake, ilikuwa na vioo kwa asilimia kubwa. Hivyo baada ya Best kuona baba yake anachelewa kurudi, alikwenda sehemu ya kutokea nje, na akiwa mlangoni, aliweza kumuona baba yake akiwa anazunguka huku na huko kama kachanganyikiwa na Dokta Ice alionekana kuzidi kumchanganya kwa maongezi yake. Dokta Boucher alikuwa kakamata kichwa chake kwa mikono miwili na kwenda huku na huko lakini Ice hakuacha kumwambia.


Ndipo mtoto Best alipotoka na kwenda hadi pale alipo baba yake na kumuulizia ni nini kinaendelea. Baba yake badala ya kumjibu, alimyanyua na kumpa tabasamu la ahueni, kisha akampooza kwa kumwambia hamna kibaya kinachoendelea.


Maneno hayo ya faraja, yakamuingia mtoto mdogo Best. Wakarudi ndani na baba yake na kuendelea kusherehekea siku ya mtoto wao kuzaliwa.

Usiku huohuo, Best aliweza kuwasikia wazazi wakifokeana huku mwanamama akitaka waondoke na baba akikataa kuondoka kwa sababu pale ndipo maisha yake yalipo. Hali ilikuwa tete usiku huo. Na si usiku huo pekee, mwezi mzima kulikuwa hamna maelewano mazuri ya baba na mama Best. Lakini mwisho wa yote, walikubali kubaki kwa msemo wa liwalo na liwe. Na ndipo usiku mmoja wenye mvua kubwa, waliingia wale mabwana ambao sasa hivi kesi yao inataka kufufuliwa upya na Limasi.


Ndani ya maono hayo, Idris aliweza kujitambua kuwa zile ni kumbukumbu zake za utotoni. Na wakati zinaendelea kujirudia, ndipo ikafika ile sehemu ya mama yake kuchinjwa kama ng’ombe wa mnadani.


“Amka Idris. Watakuua hawa mabwana. Amka.” Sauti ilisikika masikioni mwa Idris akiwa kalala pale chini na wale wanajeshi wanamichezo, kila mmoja akimpiga kwa mateke mazito na ya nguvu nyingi. Kwenye maono yake, aliweza kuona mama yake aliyekatwa shingo, akiongea maneno hayo angali damu zinaendelea kumtoka. “Inuka pambana Idris.” Maneno yalimtoka mama yake na ghafla picha ikabadilika na kuja ya Dokta Ice.


“Wewe ni mwanajeshi bora kupata kutokea kwenye uzao wetu. Hamna ambaye anaweza kusimama na wewe uso kwa uso. Utamuondoa duniani.” Dokta Ice aliongea akiwa katika mavazi meupe.


“Amka mwanangu, pambana.” Baba yake naye alitokea pembeni na kumsihi kuamka ili apigane na wale wanajeshi ambao sasa walikuwa wametulia kumpiga na kuhema kwa nguvu huku wakisubiri amri nyingine toka kwa mkuu wao.


“Amka Idris.” Sauti kali ya mama yake ilipenya masikioni mwake na ghafla alifungua macho yake kwa pamoja. Akawa karudi duniani baada ya muda kidogo kutoweka kwa sababu ya sumu iliyokuwa inasambaa mwilini mwake kwa kutumia zile sindano zilizomuingia.


Idris akatoa yowe zito baada ya kufumbua macho. Yowe ambalo alilitoa, halikukata kwa dakika moja nzima. Mwili wake ukaanza kubadilika na kuwa mwekundu kama moto. Sindano zilizokuwa zimemuingia, zikaanza kujichomoa na kusababisha wale wanajeshi wanamichezo kuanza kurudi nyuma kwa hadhari kubwa.


Idris akaamka kama mzuka huku macho yake yakiwaka kama taa zinazofungwa kwenye viwanja vya mpira. Merice akiwa chini naye hajiwezi baada ya kupigwa sana, alitabasamu baada ya kuona mwanaume yule karudi duniani. Ni sauti yake ndiyo ilikuwa inamuhasa Idris aamke na si mama yake wala baba zake, ila kichwani mwa Idris, aliona ni watu hao.


Kwa nguvu za ajabu, Idris alianza kuwakimbilia wale wanajeshi ambao walichomoa silaha zao tayari kwa kumdhibiti.


“Unatakiwa kumdhibiti mcheza mpira. Yule ndiye kila kitu.” Alikumbuka Merice aliyomwambia kama anataka kuwashinda wale wanajeshi. Na wazo hilo alimua kulifanyia kazi.


Maradona, yule mcheza mpira wa miguu. Alifanya manjonjo yake na mpira ukajitokeza mikononi mwake na kisha akaurusha kidogo juu ili aupige shuti kumuelekea Idris. Lakini ghafla Idris alipotea na sekunde hiyohiyo, akatokea mbele ya Maradona huku kaukamata mpira ambao haukufika mguuni kwa mwanajeshi yule. Akatumia mpira ule kama ngumi kwa kumpiga nao kifuani na kumuacha nao akiwa kaushikilia pale kifuani huku karushwa mbali kwa sababu ya ngumi mpira aliyokumbana nayo.


Mpira ule, Idris aliupandikiza bomu dogo sana ambalo lililipuka baada ya Maradona kutua chini. Mpira nao bila hiyana ukamlipukia Maradona na kumfanya apoteze uwezo wake wa kupigana japo hakufa. Wakati hayo yakiwashangaza wale wanajeshi wengine, Idris yeye alikuwa anapotea na kutokea tena mbele ya wale wengine na kuwapa kipigo cha mbwa mwizi. Hali iakabadilika ghafla. Idris ndiye akawa kaukamata mchezo.


Akiwa kama kapagawa, akiwapa kichapo wale wanajeshi wa Uzo, mara ilihisi kitu kikiingia shingoni kwake. Na haraka akakishika na kukitoa. Ilikuwa ni sindano na alipotazama ilipotokea, aliona sura ya Uzo ikiwa juu ya gari ambalo lilifunuka kwenye dari lake na kuacha upenyo wa mtu kutokeza. Idris akajikuta anapata hasira hasa baada ya kukumbuka kuwa yule ndiye hasa aliyeimaliza familia yake hadi leo hii mambo ya dunia yanampita.


Akataka kujitikisa kidogo, sindano nyingine ikaingia kwenye paja lake. Nguvu taratibu zikaanza kumuishia, wekundu ambao ulikuwa umejitengeneza, ukaanza kupotea taratibu. Alipojaribu kupotea, alijikuta akitokea mbele ya gari la Uzo, na saa hiyohiyo akapokea sindano nyingine ya kifuani kwa kutumia bunduki maalumu aliyokuwa kakamata Uzo.


Hali ikawa tete kwa mwanajeshi yule. Na wakati huohuo, wanajeshi wanamichezo walisimama wima na kutoa dhana zao za kimichezo. Mwenye kitenesi cha tenis, alikitoa na kukipiga kwa fimbo yake yenye nyavu. Kitenesi kile kikiwa bado hakijamfikia Idris, kikachoka sindano nyingi ambazo zilikwenda na kujikita ndani ya mwili wa Idris na kabla hajageuka, sindano kadhaa zikatoka kwenye kile kitenesi kilichonatia kwenye mwili wa Iwake na kwenda moja kwa moja kwenye nyavu ya fimbo ya tenisi. Mwanadada mcheza tenisi, akabonyeza kitufe fulani kwenye fimbo ile na zile sindano zilizonata kwenye nyavu, zikatengeneza umeme ambao ulimuingia Idris kupitia mawasiliano ya kitenesi.


Idris Iris akajikuta anapata kitetemeshi kikubwa cha mwili baada ya shoti kali ya umeme. Alipiga goti moja na kung’ata meno yake kwa maumivu makali ambayo alikuwa anayapitia kwa wakati ule. Pale alipotaka kunyanyuka, mwanajeshi mwenye viatu vya matairi alitoa kichuma chake mfano wa kifuniko kidogo cha mafuta na kukiweka chini kisha kukipiga kichuma kile. Nacho kikaenda kunasa shingoni kwa Idris kisha kikatuma waya mwembamba sana uliyokuja kunasa kwenye fimbo ya mwanajeshi mwenye viatu vya matairi. Naye bila huruma, akabonyeza fimbo yake ambayo ilipeleka umeme kwenye mwili wa Idris. Ikawa tatizo zaidi kwa Idris ambaye alikosa msaada hata toka kwa Merice ambaye alikwishapigwa pingu za shoti ya umeme muda mrefu sana.


Idris kila alipotaka kunyanyuka, wanajeshi wanamichezo walituma vifaa vyao ambavyo vilinasa kwenye mwili na kusababisha maumivu makali yatokanayo na umeme unaomwingia. Mwanajeshi mcheza rugby, yeye ndiye alikuwa kwenye pigo la mwisho. Akiwa anaurusha mpira wake juu na kuudaka kiustadi, alionekana yupo tayari kumuangamiza mwanajeshi aliyemchakaza vibaya Maradona.


Mcheza rugby aliurusha mpira wake kwa nguvu kumuelekea Idris na wakati huohuo, alikuwa kama anaukimbilia mpira wake. Mpira ule ukatua mgongoni kwa Idris na kulipuka mlipuko wa kawaida lakini ukitoa upepo mkali na kumfanya Idris achomoke mwenye zile shoti za wachezaji na wakati yupo angani, mcheza rugby alimkumba vibaya sana na kutua naye chini hadi sehemu ile ya rami, ikatengeneza shimo lililotokana na ule mshindo wa wale watu wawili. Idris macho yakamuingia giza, na kujikuta yanafunga yenyewe. Sindano za Uzo, shoti za wanajeshi na pigo la mcheza rugby, zilitosha kumtoa mchezoni Idris na wakati huo sauti ya kusikitika toka kwa Merice, ilisikika.


“Mleteni kwenye gari.” Uzo aliongea huku anaingiza mwili wake kwenye gari toka pale ambapo alichomoza nusu ya mwili wake.

Wanajeshi wanamichezo wakaenda hadi pale alipodondokea Idris na mcheza rugby, wakampongeza mwenzao na kisha kumchukua Idris kwa kumburuza hadi ndani ya gari alilokuja nalo bosi wao.


“Umekwisha mwanajeshi.” Uzo aliongea baada ya mwili kuingizwa ndani ya gari na yeye kumpiga pingu za kisayansi kwenye mikono na miguu yake. Baada ya dakika mbili, aliingizwa Merice naye akiwa hoi kwa kipigo. “Na wewe nawe unaenda kufa.”Aliongea Uzo na kufunga mlango wa gari baada ya wale wanajeshi wengine kukwea ndani ya gari hilo mfano wa Noah. Dereva akalizungusha vema na kuanza kuelekea alipotoka.


Walati wanaondoka eneo lile, pikipiki moja ilikuwa inakuja kasi mbele yao na kuwafanya wale wanajeshi kumakinika zaidi na mtu wanayemuangalia. Alikuwa kavaa nguo nyeusi, pamoja na kofia ya rangi hiyohiyo lakini pikipiki ikiwa nyekundu. Mtu yule alikuja kwa kasi na kuzidi kuleta taharuki ndani ya gari la Uzo.



Dereva wa gari hakuonekana kusita kwenda mbele na alikuwa tayari kumkumba mtu mwenye pikipiki kwa gharama yoyote na hakuna ambaye angekataa hali ile kwa sababu mwenye pikipiki alikuwa anapita eneo siyo lake.


Pikipiki iliendelea kuja kwa kasi na ilipofika karibu, hatua kama tano ili kufikiana, pikipiki ile ilipinda upande wa kushoto nakupita kwa kasi ubavuni mwa gari iliyombeba Idris huku hata koti la leiza alilovaa mwendesha pikipiki, likigusa ubavu ule.


Uzo alichomoa kichwa chake dirishani na alishuhudia yule bwana akititia toka eneo lile na yeye kujikuta akishusha pumzi ndefu ya ahueni kwa sababu hali ilikuwa tete kwake hasa alipofikiria uwepo wa baadhi ya watu kwenye ile vita.


“Nilidhani ni The Lens kafufuka.” Aliongea huku akikaa vema kwenye kiti chake.


“Yule si kitu, tulikwishamuondoa muda sana mchezoni.” Maradona ambaye alikuwa tayari kapatiwa matibabu, aliongea kwa tambo ndani ya gari lile na wengine wakacheka kwa kumuunga mkono kauli yake.


“Hapana. Mshukuru MUNGU mmefanya kazi bila yeye kutokea.”Uzo aliongea. “Nina taarifa kuwa yupo duniani, lakini sijui yupo wapi.” Akaendelea na wakati huohuo, alifungua mkoba (dashboard) au droo ya gari ile na kutoa bahasha moja kubwa. “Hizo picha zimepigwa wiki iliyopita. Alionekana maeneo ya Los Angeles, kwenye supermarket fulani huko.”Aliwakabidhi baadhi ya picha wanajeshi wale toka kwenye bahasha, nao wakaanza kuzipitia zile picha moja baada ya nyingine.


The Lens, kama Uzo alivyomuita, alikuwa ndiye yule bwana aliyeitwa Agent Unknown wa Jijini Texas. Bwana ambaye nyumba yake inamlango wa ajabu nyuma ya jokofu lake la vinywaji.

“Bosi mbona hukutuambia hili?” Mcheza tenisi, mwanadada aliongea kwa sauti ya jazba na kumfanya Uzo amuangalie kwa macho makali. Mwanadada yule alijikuta anarudisha mgongo wake nyuma na kutulia kama mwanzo.


“Kama ningewaambia uwepo wa huyu mbwa, basi msingeweza kupambana na huyu pumbavu. Akili zenu zingekuwa zinamuwaza The Lens. Mngeshindwa kazi mapema sana. Huyu naye si mwanajeshi wa kubeza, si mnaona alivyotaka kuwazimisha pale?” Uzo aliongea huku akimtazama Idris ambaye hakuwa na chembe ya uhai wala fikra za kuwepo duniani.

Wanajeshi wanamichezo wakaamua kukaa kimya huku nyuso zao zikisononeka baada ya kugundua uwepo wa mtu ambaye wanamuita The Lens.


MIEZI MITANO NYUMA.


Vita ya maneno kati ya nchi za Ujamaa na nchi za Ukabaila, bado ilikuwa zinachukua nafasi kubwa sana duniani. Nchi kama China, Korea, Urusi, Cuba na zingine, zilikuwa ni nchi zinazojiendesha kiujamaa kwenye mwamvuli wa Udikiteta na Ukabaila. Na wakati huohuo, nchi nyingi za Ulaya kama vile Uingereza, Hispania, Ubelgiji zilikuwa zinaendesha nchi zao kwa sera za Ukabaila na huku nchi yenye nguvu duniani, Marekani, ikiwapa mkono wanaotawala kwa Ukabaila.


Katika vita hiyo baridi, ndipo kila nchi ilianza kuonyesha uwezo wake wa kijeshi kwa kubuni silaha mbalimbali za maangamizi na kuzijaribu maeneo mbalimbali duniani na kurusha video kadhaa kwenye mitandao ili kuwatisha wapinzani.


Marekani na washirika wake, ndio walikuwa kichecheo klikubwa cha utengenezaji wa silaha ambazo zilikuwa zinatishia sana amani ya nchi ambazo ziliingia naye kwenye vita baridi.

Dokta Simeria, alipewa kazi ya kutengeneza silaha mpya za C.O.D.EX na ndipo alikuja na mpango wake wa muda mrefu wa kuwaunda Pro. C.O.D.EX. Mpango ambao ulikwishaandikwa zamani sana na mwanamama huyu na alishawahi kuuzungumza lakini alipewa muda wa kuwabuni zaidi ili wawe imara, na hilo likafanyiwa kazi na kufanikiwa kwa asilimia tisini na nane.


Baada ya kuwaunda wanajeshi wanamichezo, ndipo wakataka kwenda kuwafanyia majaribio ili kuona kama watafanya kazi ambayo wanatakiwa kuifanya mbele yao. Ndipo walipopata habari ya majaribio ya silaha zingine za Kisayansi katika bara la Antarctica, bara ambalo linasifika kwa kuwa na baridi kuliko bara lingine lolote duniani. Ni bara ambalo hamna binadamu wanaoishi kwa sababu ya msimu mzima wa mwaka kuwa barafu pekee.


China iliamua kwenda kufanya majaribio ya silaha zake huko na ilipeleka silaha zake mpya mbili ambazo wao waliamini kuwa ndizo uzao mpya wa silaha za maangamizi. Marekani nao wakaamua kupeleka wanajeshi wao huko wakiwa wamewajaza hali ya kutokuwa na ubinadamu bali uwezo wa kuhimili hali yoyote ya hewa pamoja ugumu wa vita watakayokutana nayo.


Silaha mbili za maangamizi kutoka China, ziliundwa kama mavazi ambapo binadamu waliweza kuyavaa na kuyatumia katika shughuli walizoagizwa. The Lens, ni silaha ambayo ilibuniwa na kupewa jina hilo na Wachina wenyewe kutokana na uwezo wa silaha hiyo ya mavazi, kuwa na uwezo wa nguvu za jua huku zikiundwa kwa vioo aina ya lens.


Silaha ya pili waliita The Storm. Ni silaha ambayo ilikuwa inaweza kumfanya mvaaji ageuke na kuwa kimbunga na wakati huohuo, kubadili hali ya hewa na kuwa mawingu magumu kana kwamba kuna mvua kubwa ya mawe inataka kuchukua nafasi eneo hilo.


Mwanadada wa Kirwanda pamoja na mwanakaka mmoja mweusi lakini hajulikani anauraia wa nchi gani duniani, ndio walipewa jukumu la kuvaa mavazi hayo ya silaha na kwenda kujaribu huko kwenye bara la barafu na baridi kali, Antarctica.


Agent Unknown na Agent R huku herefu ya R ikiwakilisha Rwanda, ndio majina waliyopewa watu hawa katika shirika la kipelelezi la kujitegemea China. Wakiwa Barani Antarctica, walikuwa wanafanya majaribio hayo ya silaha kwa kubomoa vitu kadhaa ambavyo vilikuwa vimewekwa kwa lengo hilo la majaribio.


Wakiwa wanafanya majaribio hayo, kwa mbali waliweza kuona ndege kubwa ya kivita ikija maeneo yao na kwa kasi sana, ikawapita na kwenda kutua mita kama mia tano toka pale walipo The Storm na The Lens.


“Tumeona badala ya kufanya mazoezi peke yenu, basi tufanye kwa pamoja ili tuone nani anajeshi imara na zuri.” Sauti ilisikika kwenye ndege ile na ilipenya moja kwa moja hadi kwa wanajeshi wa China ambapo sauti hiyo iliingia kwenye vichwa vyao na kusafiri hadi makao makuu.


“Hatuhitaji hitaji lako, tupo vema kwa hapa tulipo.” The Lens aliongea maneno ambayo aliambiwa haijibu ile sauti toka kwenye ndege kubwa ya kivita.


“Mnadhani hayo mnayoyawaza, na hawa hapa wanayawaza?” Mlango wa ndege ile ulifunguka na kisha wanamichezo sita walitokeza, huku mwanajeshi mmoja pekee akiwa kaongezeka kati ya wale watano waliopambana na Idris na Merice.

Mmoja huyu aliyeongezeka alikuwa mwanadada mwenye mwili mdogo kiasi, na alifunga nywele nyuma na kuvaa mavazi meupe, na mkanda mweusi kiunoni, yakiwa ni mavazi maalumu kwa ajili ya mchezo wa kung fu na kareti.


“Hatuhitaji vita Uzo.” Sauti ilisikika tena toka kwa The Lens, ambaye mavazi yake yalikuwa kama vyuma lakini yaliyopendeza hasa kwa rangi yake nyeusi. The Lens alikuwa na mwili mkubwa kuliko wale wanajeshi kutokana na yale mavazi. Viganja vyake vya mikono vilitapakaa lens kali sana inayoweza kutandaza mionzi mikali ya nyuklia inayojitengeneza mwilini mwa vazi lile huku likishindwa kumdhuru mvaaji


“Najua hamuhitaji vita, ila hawa wapo majaribio.” Maneno hayo yalienda sambamba na wale wanajeshi sita wanamichezo, kujipanga mstari na kuweka silaha zao za kimichezo tayari kwa kuwavamia.


“Sawa, ngoja tuone mlichobarikiwa.” The Lens aliongea kwa sauti ya chini lakini ilimfikia vema The Storm ambaye naye alikuwa kavaa mavazi mepesi mithili ya yale ya Kihindi lakini yamebarikiwa kuwa na Sayansi ya aina yake endapo yakihisi hatari. Usoni kwake huyu mwanadada, alikuwa kavaa kinyago cheusi kinachomuwezesha kuona na kuvuta hewa kwa ufasaha bila kudhurika.


Alikuwa ni Maradona, yule mcheza mpira aliyeanzisha vurumai baada ya ndege iliyowaleta kuondoka. Aliupiga mpira wake kwa nguvu kumuelekea The Lens lakini Lens hakufurukuta bali kusogeza kidogo mwili wake na mpira ule kupita.


“Hapo ndio mwisho wako dogo?” Akauliza Lens baada ya mpira ule kutokuwa na madhara. Lakini kabla hajajibiwa swali lake, mpira ule ulimrudia toka nyuma lakini suti yake aliyoivaa, iliweza kuhisi ujio huo, hivyo mikono yake ikatoa muhale mkali uliyoteketeza mpira ule kabla hujamfikia. “Nadhani hilo ndilo ulilokuwa unalitegemea.” Akamwambia baada ya mpira ule kugeuka moto.


Wanajeshi wachezaji wakaangaliana, na kisha kwa pamoja walianza kufanya mavamizi yao ya kimichezo lakini The Lens pamoja na The Storm, waliweza kuwadhibiti vema bila wao kutumia silaha. Kila wanamichezo walipojaribu kupambana, waliambulia kupigwa vibaya sana.


“Mimi nashauri muite ndege yenu, muondoke hapa kabla hatujaanza kufanya yetu.” The Storm alifunguka uso wake na kuongea hayo huku akiwa anawaangalia wale mabwana wanavyotweta kwa nguvu baada ya kuchoka.


“Tumekuja kufa huku, hatujaja kufukuzwa na nyie mbwa.” Aliongea mcheza rugby kwa hasira.


“Ohoo! Basi sawa.”The Lens alitabasamu na kukubaliana na wale mabwana. “Storm, waonyeshe.” The Storm alifunga uso wake na kisha akiwa palepale, akanza kuzunguka kwa kasi na kuanza kutengeneza kimbunga kikali sana.


Baada ya dakika kadhaa, kimbunga kilikuwa kikubwa na kilikusanya asilimia kubwa ya Barufu. The Lens akiwa mbali na The Storm, suti yake yote ilibadilika na kuwa ya kioo na kisha kutengeneza miale mikali ya nyuklia au jua ambao ulitoka mwilini mwake na kuingia ndani ya kimbunga kile ambacho nacho kilichukua miale ile ya jua toka kwenye mwili wa The Lens, na kutengeneza moto mkali wa kimbunga.


Kimbunga kile cha moto, kikaanza kuwafuata wanajeshi wa C.O.D.EX kwa kasi na kila kilipozidi kutembea, ndivyo kilizidi kuwa kikubwa. Wanajeshi wanamichezo, walikumbwa na uoga mkubwa sana. Na kabla kimbunga kile hakijawafikia, ndege iliyowaleta ilitokea na kurusha bomu kubwa sana kwenda kwenye kile kimbunga.


“Hapanaaaa…” The Lens alipiga ukelele mzito baada ya bomu lile ambapo lilipotulia, The Storm alikuwa chini kalala huku damu zikimtoka kila mahali. The Lens alikimbia hadi pale na kumuangalia na kisha kuangalia ndege ile ilipo. Akajikusanya nguvu, na kurusha miale mingi ya nyuklia toka mwilini mwake lakini ndege ile ya kijeshi ilikwepa.


Ndipo alipoamua kuwageukia wale wanajeshi wachezaji, lakini kwa bahati mbaya, miale yake ilikuwa imekwisha na inatumia dakika zipazo kumi ili kujikusanya tena. Ikabidi achomoke toka kwenye ile suti na kushuka chini yeye mwenyewe kwa ajili ya kupambana nao wale wanajeshi uso kwa uso.


Alikimbia kwa kasi kuwaelekea wanajeshi wa C.O.D.EX na wakati huohuo, mwanajeshi mwenye viatu vya matairi na vyenye uwezo wa kutereza kwenye barafu, naye alikuwa anamfuata kwa kasi ileile akiwa kakamata fimbo yake ya michezo. Walipokaribiana, The Lens alichana msamba mkali na kuacha nguo zake zimsaidie kutereza na wakati huohuo, akaachia ngumi kali sana iliyomkuta mwanajeshi kwenye ubavu wake, huku yeye fimbo yake ikipiga hewa.






Mwanajeshi yule alijikunja tumboni na kuruka hewani kama njiwa aliyepigwa risasi, na kisha kutulia mgongo. Wale wenzake walipoona hivyo, ikabidi wajipange kumshambulia The Lens lakini, walikuwa wamekwishachelewa.

Mcheza Rugby, ambaye yeye alikuwa tayari kuurusha mpira wake kwa nguvu nyingi sana, alikutana na upinzani mkubwa wa mkono mmoja wa The Lens ambaye aliuzuia mkono ule ukiwa angani tayari kwa kuurusha mpira. The Lens alimtazama Mcheza Rugby kwa macho makali na wakati huo yule mwanajeshi akiwa analazimisha kuukandamiza mpira wake kwenye mkono wa The Lens.

“Nakuua leo. Na baada ya wewe, nawaua na wenzako kisha namuua na baba yako aliyekutengeneza mbwa wewe.” The Lens aliongea kwa kisirani na yule mwanajeshi aliacha kuhangaika kujipapatua kuukandamiza mpira wake ambao ni kama alikuwa anashindana nguvu na mkono mmoja wa The Lens ambaye aliuzuia mpira ule pale mkononi kwa Mcheza Rugby ukiwa angani.

Mwanajeshi alimtazama The Lens usoni na aliona kuna sura ya mauaji pekee na kabla hajafikiri afanye nini, The Lens aliuvutia mpira kwake na kuukamata mkononi na kumfanya Mcheza Rugby aduwae kwa tukio lile. Na kabla hajaduwaa zaidi ya pale, The Lens alimpiga vibaya sana kwa mpira ule eneo la sikio lake.

Pigo lile lilikuwa kama ‘ngumi mpira’, yaani The Lens alimpiga na mpira ule sikioni bila kuuachia mpira. Mcheza Rugby akaona maruwe ruwe, akajihisi kama anataka kudondokea upande wa pili wa sikio ambao haukupigwa ngumi mpira, lakini alijikuta anarudi alipokuwepo kwa kupigwa ngumi nyingine nzito ya sikio la upande mwingine, akapofuka masikio.

Na wakati huo The Lens alimuachia karate matata sana kwa kumpiga kwa vidole vyake shingoni. Akawa kamziba hewa na mwanajeshi yule akawa anarudi nyuma huku kakamata shingo yake. Na hakurudi nyuma pekee, alisindikizwa kwa mpira wake wa kasi kutoka kwa The Lens ambao mpira ule ulitua tumboni kwake na kumrusha hadi kwa wenzake ambao walikuwa hawaamini kama jitu kubwa kama lile, linazuiliwa na mtu mwenye mwili mdogo tu.

Kwa hasira, mwanadada aliyekuwa kavalia mavazi ya kuchezea mchezo wa kung fu na karate, aliruka sarakasi kadhaa kumwendea The Lens na wakati huo The Lens alikuwa anarudi kidogo kidogo. Mwanadada mcheza karate, alifika karibu na The Lens na kutua kwa miguu miwili kisha akarusha mateke kadhaa ambayo The Lens aliyetolea nje kiustadi. Mateke yalipoanza kuisha, mwanadada yule akaanza kurusha ngumi.

Wakati ngumi hizo zinarushwa, saa ya The Lens ikaonesha kuwa zile nguo zake zimejaa nguvu. Akaibofya saa yake na mara kiganja cha mkono toka kwenye ile suti kilienda hadi mkononi na kujivaa. Yule mwanadada mrusha ngumi, alishangaa anadakwa mkono wake kwa mkono wa chuma na baadae chuma kile kilitoa muale mkali wa jua na kumkata kabisa mkono yule dada.

Mwanadada alipiga yowe la uchungu lakini haikuwa sababu ya The Lens kumuacha. Alimgeuza haraka na kuwa kama amemkaba kwa nyuma, kisha kwa mkono uleule uliyovaa chuma, akamuwekea shingoni na kwa nguvu sana, akalivuta koromeo la yule dada na kulitupia pembeni. Na kabla yule mwanamichezo hajadondoka, mkono ule ukawa kioo ambacho kilitumika kukata kabisa shingo ya yule mwanadada. The Lens akabaki kashika nywele za kichwa cha mwadada huku kichwa chenyewe kikining’inia na kiwiliwili kikidondokea tumbo.

“Pumbavu.” Maradona, yule mcheza mpira alijikuta akitukana na kuanza kusogea mbele lakini alisita baada ya kuona nguo za The Lens zikianza kujivaa mwilini. Kwa haraka, wale wanamichezo walijipanga mstari mmoja na kushikana mikono. Kisha nguvu nyingi sana zilianza kuwatoka mwilini na kusababisha tetemeko ambalo lilianza kubomoa ardhi ya barafu. Na ghafla nguvu zile ziligeuka na kuwa mlipuko mkubwa ambao ulifanya eneo lile kugeuka kuwa maporomoko ya barafu.

Ndege iliyowaleta, ilifika haraka walipokuwepo wale mabwana na kutua juu yao kama vile inawavaa, na ilipoinuka, kulikuwa hamna wanajeshi. Ngege ikapotea huku The Lens akijitahidi kuogelea kutoka mle chini ya barafu alipotumbukia baada ya mlipuko ule. Lakini hakuweza kujiokoa na hata nguo zake za mapigano, hazikuweza kumsaidia kwa sababu zilikuwa zimeundwa kwa mtindo wa jua na kitu chochote chenye asili ya jua/moto, hakipatani na maji. The Lens taratibu akaanza kuzama ndani Zaidi ya eneo lile huku kanyoosha mkono wake angani kama mwenye kutaka msaada ili mtu amuokoe. Na wakati huo, The Storm naye alikuwa anazama baada ya kifo chake kuchukua nafasi mapema sana.

Wale waliyokuwa ndani ya ndege, walishuhudia hali ile. Walisikitika hasa pale walipokumbuka kisanga kilichompata mwanajeshi wao mcheza karate. Walimuona naye akizama ndani ya maji akiwa hana kichwa.

“Mashujaa hufa kifo kibaya kuliko watu wowote wale.” Aliongea Mcheza Rugby baada ya kuona miili ile ikizama. Alikubali kuwa wale walikuwa mashujaa ambao walijitokeza kwenye maisha yake.

****

Gari lililokuwa limewapakiza Uzo na wanajeshi wake pamoja na Idris na Merice, lilifika makao makuu ya C.O.D.EX na kwa haraka, wanajeshi wale walishuka na kisha kumtoa Idris ambaye alikuwa kafungwa pingu kwa nyuma na pingu hizo, zimeunganika na pingu zingine miguuni kwake na kufanya Idris kuwa kama mnyama mkubwa wa porini aliyeuawa na kisha kuning’inizwa mwenye fimbo kubwa, kisha kubebwa na wawindaji hao mabegani.

Idris ambaye alikuwa hana fahamu, alitolewa ndani ya gari na kuanza kuburuzwa kama kitu kizito kilichochokwa kubebwa na wahusika. Merice naye ambaye alikuwa anafahamu zake, alitolewa ndani ya gari lile na kuanza kupelekwa ndani ya maabara ile kubwa kwa kusukumwa.

“Karibu mwanangu.” Simeria, mama wa Merice aliongea huku katabasamu na kumfuata Merice ambaye alikuwa hana chembe ya furaha usoni kwake.

“Nimeletwa nikuue tu, mbwa mkubwa we.” Merice aliongea kwa hasira na kumfanya mama yake azidi kutabasamu.

“Usijali mwanangu, najua umejazwa ujinga na huyu paka shume,” Aliongea huku anamtazama Idris aliyekuwa anatolewa nguo zake baada ya kufunguliwa pingu. “Hapa utarudi kwenye hali yako ya zamani, na utakuwa mwanajeshi ambaye utasikia amri zetu tu!” Akaongeza Simeria.

“Hutonipata tena.” Merice naye alijibu kwa uhakika bila kuogopa.

“Sawa. Ngoja tuone,” Akaongea Simeria. “Mpelekeni kwenye jokofu lake.” Akatoa amri, na madaktari kadhaa wakiongozana na wanajeshi wenye silaha, walikuja kumchukua Merice na kwenda naye hadi eneo ambalo Idris alikuwa anaandaliwa tayari kwa kuingizwa kwenye vifaa maalumu kwa ajili yake.

****

Huko Texas, bwana ambaye aliitwa Agent Unknown, aliweza kupata taarifa ya gari la Uzo lilipokwenda baada ya pikipiki nyeusi iliyokuwa inaendeshwa kwa kasi na mtu ambaye hakuonekana uso wake, kupishana na gari hilo. Bwana ambaye alikuwa juu ya pikipiki, aliweza kupandikiza kitu kidogo sana kwenye gari lile. Kitu hicho ilikuwa ni ngumu sana kuonekana na mtu mwingine au mitambo yoyote ile.

Baada ya kitu kile kupandikizwa, saa ya Agent Unknown iliwaka mwanga mwekundu na kisha kuonesha dira na kialama cheupe ambacho kilisimama kama gari la Uzo.

“Baada ya siku tatu nitakuwa hapo wazee. Mjiandae tu.” Aliongea Agent Unknown baada ya kushuhudia mwisho wa alama ile ambapo ilikuwa ni pale makao makuu ya C.O.D.EX

Nchini Tanzania, Limasi na kundi lake walikwishaanza mchakato wa kupitia video na nyaraka mbalimbali alizokuwa ameacha Idris. Walikuwa katika hali ya kufanya kazi kuliko kipindi kingine chochote. Nyumba ya Idris ambayo ipo Arusha, na ambayo Limasi na Idris walikuwa wanaishi, ndio ilikuwa kambi maalumu ya wanasheria wale kukaa kwa pamoja na kuijadili ile kazi ambayo waliitiwa toka kwenye nchi zao.

“Hii kesi ni lazima tuipeleke Kimataifa.” Mwanadada mmoja abaye alikuwa anaasili ya Kihindi, aliwaambia wenzake huku kakamata karatasi ambayo ilikuwa inamaelezo mengi sana juu ya Idris.

“Umeona eeh, Chameli, hapo lazima ifike hadi mahakama za kimataifa ili wakione cha moto hawa.” mwanadada mwingine, aliitwa Brighita, anaasili ya Brazil, alimuunga mkono mwanadada wa Kihindi. Chameli.

“Tujitahidi tu wapendwa. Hapa lazima tutapata sana msaada.” Faruq Omary, kijana wa kiume toka Iran, naye hakuwa nyuma kuungana na wenzake aliosoma nao huko India masomo ya sheria.

“Na tukifanikiwa kushinda hii kesi, nadhani dunia kwa ujumla itakuwa inatutazama sisi kwa macho ya tisa.”Buja Bujiku, Mnaijeria mwenye ucheshi mwingi aliongeza.

“Macho ya tisa?” Akauliza mwanadada mwingine, yeye aliitwa Theresa Tyrese, Muingereza mwenye asili ya weusi. Alikuwa anacheka sana baada ya kusikia macho ya tisa. “Yaani wewe nilikumiss hapo tu kwenye ucheshi wako.” Akaongeza na wakati huo wote walikuwa wanacheka.

“Mmenikumbusha sana shule jamani. Yaani najihisi kama bado nipo chuoni, kila napowatazama.” Limasi aliongea huku anawatazama mmoja baada ya mwingine. “Ahsanteni sana kwa kuja kufanikisha hii kazi.” Akawashukuru.

Watu hawa sita ndio walikuwa kundi bora la wanachuo katika mwaka waliomaliza chuo huko India. Kundi hili la kujisomea, liliundwa kwa kuunganisha mataifa sita tofauti, yaani India, Uingereza, Naijeria, Tanzania, Iran na Brazil. Na ndilo kundi lililokuwa linawatu toka mataifa mbalimbali bila kuchagua dini na rangi zao. Walishinda kundi bora la chuo katika masomo ya Sheria, na sasa, wapo pamoja tena katika kutimiza ndoto na malengo yao ya kimaisha. Wapo tayari kupigania kesi ngumu ya Idris.

”Limasi, kila wakati tunajaliana. Hiyo ndio kauli mbiu yetu. Au umesahau?” Mbrazil, Brighita, alimwambia hayo Limasi huku anampigapiga begani kwake.





Baada ya kukusanya kila kitu vema, Agent Unknown, alikwenda haraka nyuma huku kaiweka bunduki yake aliyoikunja upande wa kushoto. Kisha baada ya kufika usawa anaoutaka, akaanza kukimbia kwenda mbele kwa kasi zaidi na kisha kupita kwenye dirisha lililokuwa wazi, na ambapo alikuwa anachungulia kila kitu kinachoendelea kule kwenye maabara ya C.O.D.EX. Aliruka toka kwenye ghorofa lile ambalo lilikuwa lina ghorofa thelathini na tano. Yeye, Agent Unknown, alikuwa ghorofa ya thelathini na tatu.

Alipojirusha, akatua kwenye ghorofa linalofuata lakini kwenye chumba cha watu ambapo alipitia dirishani na kuvunja kioo cha chumba kile. Ndani ya chumba hicho, alikuta watoto wawili wanacheza kwa pamoja na midoli yao.

“Hamjambo watoto?” Unknown aliwasalimia na watoto wale wakajikuta wanafurahia hasa baada ya kuona mavazi ya Kikomando ya Agent pamoja na bunduki ambayo ilikuwa bado inaning’inia.

“Hatujambo shikamoo kamanda.” Wakasalimia nao watoto huku wakiwa wanatabasamu.

“Oooh! Nimelipenda hilo jina.” Unknown aliongea na kujipekua mifukoni na kutoa boksi dogo la bazuka na kuwapatia. “Mama na baba wapo wapi?” Akawauliza tena.

“Wametoka.” Wakajibu kwa pamoja.

“Wakija mtawapa hii hapa ili watengeneze dirisha. Sawa eeh. Na nyie msicheze tena humu, nendeni sebuleni.” Akaongea huku anawakusanya na kuwapa noti tano za dola mia moja kila moja.

Watoto wakatoka mle chumbani na midoli yao pamoja na bazuka. Unknown akachomoa ufunguo wa chumba kile na kufunga kwa nje. Kisha akabomoa kitasa kile ili wale watoto wasiweze kufungua hata kama wataupata ufunguo.

Baada ya kuhakikisha usalama wa wale watoto upo, akachomoka na kuingia hadi sebuleni kwao. Huko aliwakuta wakifurahia bazuka na mchezo wao wa kupiganisha midoli.

“Natokea hapa watoto eeh.’ Akawaambia na wakati huo anafungua dirisha kubwa la sebuleni hapo.

“Sawa Kamanda.” Unknown alichomoka mwili wake kwenye dirisha lile na kisha alilifungua kwa nje. Watoto wakawa hawaamini wanachokiona. Agent unknown akatizama chini. Ulikuwa ni umbali mrefu sana kuruka. Lakini yeye hakutazama chini kwa sababu ya umbali, alitazama chini kuona kama mali yake ipo salama.

Akaona kuwa ipo vema. Akajirusha na wakati huo watoto walitoka kwa kasi na kwenda kuchungulia. Hapo walimuona Agent akiwa kafungua parachuti na moja kwa moja akenda kutua kwenye gari moja la gharama sana, na ambayo ilikuwa wazi. Na wakati huohuo, akiliondoa parachuti lake mwilini.

“Woow. Kamanda ni hatari sana” Wale watoto walifurahi walichokiona na wakati huo, Unknown aligeuka na kuangalia alipotoka. Kulikuwa ni mbali sana, alakini alihisi kuwa wale watoto wanamuangalia, akawaonyeshea dole gumba. Japo wale watoto nao walikuwa hawana uhakika kwa kile kitendo, walimpungia mkono Kamanda wao.

“Muda wa kazi.” Akawasha gari lake la gharama na kwa kasi sana akaanza kuliondoa pale na kuzidi kusababisha mshangao mkubwa kwa watu waliokuwa wanamuona tangu anafika pale chini kutoka juu ya ghorofa la thelathini.

Safari yake alionekana anaelekea yalipo makao makuu ya C.O.D.EX hivyo ulinzi wa eneo lile ukaongezwa kwa kufungwa mageti yake na wanajeshi kadhaa kujiweka sawa na mitutu yao yao ya bunduki.

Unknown alipoona kuwa ulinzi umewekwa zaidi kwenye geti la makao makuu ya C.O.D.EX akatabasamu na kisha akabonyeza vitufe fulani kwenye sehemu ya usukani wa gari lake. Mbele ya gari lile kukatokea ngao kubwa sana. Naye Agent akaongeza kasi ya gari lake na alipofika getini, alilikumba geti lile kubwa na gumu na kulivunjilia mbali. Akaingia ndani kwa ubabe mkubwa na wakati huo risasi zilikuwa zinamiminika toka kwenye bunduki za walinzi. Hakujali kwa sanabu gari lile lilikwisha jifunga juu na halikuweza kuingiza risasi.

Msele mkubwa ukapigwa eneo la ndani ya makao makuu ya C.O.D.EX na Unknown alitazama juu ambapo anatakiwa kwenda. Walinzi wa eneo lile waliendelea kupoteza risasi huku Agent akiwa wala hana fikra juu yao, yeye alikuwa anawaza ni vipi atafika walipokuwepo wakina Uzo.

Katika hali ambayo hamna aliyeitegemea, Agent Unknown, alibonyeza vitufe kadhaa kwenye sehemu ambapo mara nyingi hukaa redio ya gari au tv (dashboard), na mara gari lile likaanza kujifungua fungua na baadaye likawa kama roboti.

“Hee! Transformer?” Mlinzi mmoja alishangaa kwa sauti wakati gari lile likibadilika na kuwa roboti. Alifananisha badiliko lile na yale anayoyaona kwenye filamu za Transformers.

“Hapana. Huyu ni The Lens.” Unknown ambaye alikuwa ndani ya roboti lile, aliongea huku anamuinamia hadi usoni yule askari ambaye alihisi haja ndogo inataka kumchomoka.

The Lens, aliangalia juu ambapo anataka kwenda. Ghorofa ya thelathini na mbili ndipo wakina Uzo walipokuwepo. Kuna umbali mrefu sana toka pale alipo. Alichofanya ni kubonyeza tena vitufe kadhaa, na The Lens akageuka na kuwa roketi, ndege yenye kasi kubwa sana. Wale walinzi ambao waliacha kushambulia lile gari, wakawa hawaamini hasa pale roketi ile ilipochomoka ghafla na kwenda juu.

*****

Ndani ya maabara ya C.O.D.EX, tendo la kuhamisha damu kutoka kwenye mwili wa Idris kwenda kwenye wanajeshi wengine watano, lilikuwa linaendelea kwenye asilimia sabini. Na ndio wakati ambao Unknown alikuwa amechomoka toka kwenye jengo alilokuwa anaaangalia kila kitu kinachoendelea kwenye maabara ile.

“Nadhani tunaelekea kufanikiwa.” Uzo aliwaambia watu kadhaa aliokuwa nao na wote walitulia wakisubiri mafanikio hayo wajionee kwa macho na si kwa midomo ya Uzo.

Asilimia mia ilifika lakini kimya kilikuwa kikubwa. Hamna ile sauti ambayo ilitegemewa kuwa itasikika ya kuwa tendo la kuhamisha damu limekamilika. Na badala ya kusikia sauti hiyo, mstari uliyokuwa unahesabu asilimia hizo, ukaanza kushuka kwa kasi kwa wale wanajeshi wanne, kasoro Merice.

Na wakati tendo hilo linatokea, Uzo alipokea taarifa kuwa wamevamiwa na mtu aliyejitambulisha kwa jina la The Lens, na alibadilika na kuwa roketi.

“Mungu wangu. Tayari tumekwisha.” Uzo aliongea huku macho yamemtumbuka kama mgonjwa wa kwashakoo.

“Nini tena Uzo?” Akauliza Jenero.

“The Lens tupo naye mjengoni. Na sasa kaimarisha silaha yake.” Akajibu na akafanya akili ya haraka kwa kuwafungulia wanajeshi wake wa michezo. Nao kwa haraka wakafika kwenye eneo husika na kujipanga mstari na vifaa vyao huku macho yao yakiwa sehemu ambayo waliamini kuwa The Lens atatokeza.

Roketi ya Unknown ilipita kwa kasi nje ya dirisha ambalo wanajeshi wanamichezo walikuwa wanalitazama. Nao hawakujua wafanye nini kwa sababu hawakujua The Lens alifanya tendo lile kwa sababu ipi.

Kimya kikiwa kimetawala na akili zao wote zikihamia kwa The Lens, mara sauti toka ndani ya maabara ile ilisikika. Ilikuwa ni sauti ya kike toka kwenye kompyuta ikisema ‘Upload Complete’, yaani kile kitendo cha kuingiza damu kwenye miili ya wanajeshi kilikuwa kimekamilika.

Simeria akatazama yale majokofu yote matano na alijikuta akipiga ukelele mkubwa sana wa kero. Majokofu yalionyesha kuwa, ni Merice pekee ndiye alifanikishiwa kuingiziwa damu ya Idris. Wale wengine wanne, baada ya kuingiziwa ile damu ya Idris, wakaanza kunyonywa tena kwa mwili wa Idris kuichukua damu yake pamoja na ile ambayo wanayo. Simeria aligundua hilo na ndio maana akapiga ukelele wa kero.

“Nini Simeria?” Uzo akabonyeza kitufe cha kusafirisha sauti toka alipokuwepo kwenda ndani ya maabara.

“Tumefeli Uzo. Tumefeli…” Simeria aliongea huku kajikamata kichwa chake na wakati huo madaktari wengine walikuwa wanahangaika kufanya jitahada za kufanya yale matokeo yasiwe yenyewe.

“Nini kimetokea?” Uzo akauliza tena kwa hamaki.

“Hamna kama Dokta Ice. Atabaki kuwa yeye kama yeye. Ni namba moja daima.” Badala ya kujibu swali, akamsifia Dokta Ice ambaye alikuwa ni mume wake wa zamani.

“Simeria. Nini kimetokea?” Uzo akauliza tena na safari hii kwa kufoka.

“Hamna kilichofanyika zaidi ya kuwapa nguvu Idris na Merice.” Akajibu kifupi.

“Nilitaka kuwaambia, mkanikatisha hapa. Nilijua kuna kitu mmekisahau kwenye uchunguzi wenu.” Dokta Boss, Mkemia wa nchi, alibwabwaja na Uzo akamtazama kwa macho ya udadisi.

“Una maana gani?” Ikabidi amuulize yule bwana.

“Ni kwamba, huu ni mpango wa huyo mwanajeshi wa Dokta Ice kumbadilisha huyo mwanajeshi wenu wa kike ili awe kama yeye. Na kukubali kuingia ndani ya maabara hii, ni kwa sababu anajua anachokifanya. Huyo mwanajeshi wa Dokta Ice, hata wangekuja wanajeshi wenu wanaocheza mipira na rugby mia tano, wasingemuweza huyo. Na ndicho kitu kilikuwa kinanishangaza, kwa nini akubali kirahisi?” Maneno yakamtoka Mkemia Mkuu.

“Tunafanyaje sasa?” Uzo akauliza kama mjinga vile.

“Tusubiri waamke na watuue tu.” Akajibu Dokta Boss na mara risasi ikatua kwenye paji lake la uso.

“Pumbavu wewe. Hamna anayekufa leo, zaidi yako.” Jenero aliongea huku akirudisha bastola yake sehemu husika na kisha mlinzi wake alimletea simu ambayo ilikuwa kwenye mkoba kama ule wa Hayati Dokta Boss. Mkoba ukafunguliwa na simu ile ikaonekana ikiwa imezungukwa na mitambo kadhaa kama mixer za studio za muziki.

Jenero akanyanyua simu yake na kubonyeza vitufe kadhaa.

“Tuletee F.O.F hapa makao makuu ya C.O.D.EX” Baada ya maneno hayo, akakata simu. Uzo akabaki mdomo wazi asielewe alichoongea Jenero.

“F.O.F?” Akajiuliza Uzo.

“Future Of Forever.” Jenero akamtajia Uzo kirefu cha F.O.F yaani kizazi kijacho cha milele.

“Ni nini hiyo?” Akauliza

“Wanajeshi wapya toka kwenye maabara mpya.” Akajibiwa.

“Sijaelewa. Maabara mpya, ipi na ya tangu lini?”

“Living Lab. Ipo tangu miezi mitatu iliyopita.”

“Mbona hamkuwahi kuniambia kuhusu hili?”

“Kwa sababu hatutumii kemikali wala maiti kuunda silaha zetu. Tunatumia kama hiyo ya Wachina kuunda silaha zetu.”

“Hata kama, ndio…..” Hakumaliza Uzo, kishindo kikubwa kikaanza kusikika juu ya paa ya ghorofa lao. “The Lens huyo.” Akajikuta anabwatuka na kitete kikimzonga usoni pake.

Baada ya roketi ya Unknown kupita kwa kasi kwenda juu, ilianza kutoboa ghorofa lile toka juu ya paa ambapo kulikuwa ni ghorofa ya hamsini. Na sasa roketi ile ikawa inaelekea ilipo maabara ya C.O.D.EX.

“Wote, sogeeni hapa.” Uzo alibwabwaja na wachezaji wake wakakimbilia hadi kule walipo na kuweka uzio ambao usingeruhusu Uzo na wenzako kudhurika kwa lolote litakalotokea.

Pindi macho yao yote yapo kwenye paa la maabara ile, huku ndani ya majokofu kulianza kulipuka na cheche zilonekana kutokea mle ndani. Hali ikawa tete kwa Simeria na wale madaktari wengine waliyokuwepo.

“Vita imeanza.” Uzo alinong’ona peke yake.






Dakika moja pekee ilitosha ndani ya maabara ile kutulia milipuko yake na kuacha moshi mkubwa ambao ulipotulia, yakaonekana majokofu ya Merice na Idris yakiwa wazi lakini, wao hawakuwepo.


Simeria akiwa anashangaa huku na huko, mara madaktari aliyokuwa nao, wakaanza kutupwa kwenye kuta ngumu za maabara ile na kupasuliwa vibaya matumbo pamoja na vichwa vyao. Damu zilijitengeneza kwenye kuta na vioo ambavyo viliizunguka maabara ile. Lakini hamna kilichoonekana kinafanya vile hadi pale madaktari wote walipo poteza uhai.


Merice akajitokeza akiwa kama anawaka moto lakini baadae alirudi katika hali yake na kuvaa mavazi ya kijeshi. Na wakati huohuo, Idris naye alijitokeza kwa njia kama ya Merice. Simeria macho yakamtoka hasa mwanaye alipoanza kumfuata pale alipo.


“Nilikwambia mama yangu, huwezi kunipata kirahisi hivyo. Umefanya kosa kubwa sana ambalo…” Merice alikuwa amefika pale kwa mama yake na kumkaba. “….. Halistahili msamaha, zaidi ya ……” Akanyoosha mkono wake kisu kirefu kikajitokeza mkononi mwake.


“Mwanangu. Unajua nakupenda sana. Nakupenda kuliko chochote kile maishani mwangu.” Simeria akaanza kujitetea.


“Najua. Na ndio maana uliniua, na kisha kunitengeza mwanajeshi nisiye na huruma. Na ukamuua baba kwa sababu ya umalaya wako, na tamaa ya kumiliki kila kitu. Lakini baba, bado akili yake hukuiweza.” Merice akamwambia mama yake huku macho yake kuna muda yakiwa yanabadilika na kuwa kama vijinga vya moto.


“Nisamehe mwanangu.” Ndilo neno aliloongea Simeria kwa shida sana kwa sababu ya roba kali aliyokuwa kakamatwa.


“Adhabu yako ni…” Merice aliingiza kile kisu kirefu nyuma kidogo ya kidevu cha Simeria, na kisu kile kikatokea kwenye utosi wa mwanamke yule. “Kifo…” Akamalizia kauli yake baada ya kumuua Simeria.


Dakika iliyofuata, kishindo kikubwa kilisikika kwenye paa la maabara ile na ile roketi ya Unknown ilijitokeza kwa kushtukiza na wakati huohuo, ikijigawa gawa vipande kadhaa. Bawa la kushoto la roketi likachomoka, na la kulia pia. Na katikati ya roketi napo kukaenda mahali pake na yale matairi yake, nayo yakachomoka kwa kasi na kwenda kugonga kioo kikubwa ambacho kilitenganisha maabara ile. Kioo kikavunjika na matairi yale mawili, moja likamfuata Merice na lingine Idris.


Merice na Idris wakajiweka mkao wa mapambano na matairi yale yalipofika karibu yao, waliyakata kwa mapanga fulani yaliyojitokeza kwenye mikono yao. Lakini walifanya kosa kubwa sana kwa sababu matairi yale yalilipuka na kuwarushia mbali na vibaya sana, huku mlipuko ule ukizidi kuvunjavunja chumba kile na kuzidi kusababisha mtafaruku mkubwa mle ndani.


Yale mabawa mawili, yalichomoka pale yalipokuwepo na kwenda moja kwa moja kwa wale wanajeshi ambao walikuwa wamewatinga wakuu wao, na kisha yaliwakumba vibaya sana kuwatupia kwa wakubwa wao. Kisha mabawa yale yalirudi eneo ambapo yalidondokea toka juu, na ile sehemu ya kati ya roketi, nayo ikajiunga na mabawa yale. Baada ya dakika ipatayo moja, roketi ilikuwa imejiunda lakini ilikuwa haina matairi. Sekunde hiyohiyo baada ya kurudi na kuwa roketi, ikajibadilisha kwa haraka na kuwa The Lens, yule roboti mkubwa ambaye walinzi walimfananisha na transformer.


Uzo akiwa chini baada ya wanajeshi wake kumkumba kutokana na msukumo wa mabawa ya roketi, aliweza kumshuhudia Agent Unknown akijitokea kwenye tobo lililotobolewa na roketi yake huku miguuni kavaa viatu ambavyo vilimsaidia kupaa au kutua chini bila kudhurika. Viatu hivyo vilikuwa vinatoa moto mdogo wa bluu (nitro) na ndio ulimfanya Agent aweze kupaa au kutua. Na moja kwa moja, sehemu ya kifuani ya The Lens, ilifunguka na yeye kuingia hapo tayari kwa kuchezesha mwili wa roboti yule.


“Nimerudi.” The Lens aliongea na wakati huohuo, wale wanajeshi wanamichezo wakamakinika zaidi na kukaa mkao wa mapambano.

The Lens akachomoka pale alipokuwepo na kuruka kuwaelekea kule walipo wanajeshi lakini alikutana na upinzani mkubwa wa bomu lililomtupa pembeni bila kuwafikia wale wanajeshi. Wote waliyokuwepo mle ndani, wakatazama ni wapi bomu lilipotokea, ndipo wakaona mkono wa Idris ukijirudi na kuwa mkono wake halisi baada ya kuwa RPG kwa sekunde kadhaa ili kumsambaratisha The Lens aliyekuja kama adui kwake.


“Pumbavu.” The Lens alibwata na kusimama tena wima kwa kutumia nguvu zaidi. Akamtazama Idris, kisha akamtazama Merice ambaye alijiunga naye sekunde kadhaa mbele. The Lens akajitoma kama anayejitoma kwenye bwawa la kuogelea. Na wakati yupo juu, akabadilika na kuwa roketi ya vita na kurusha mabomu kadhaa toka kwenye mbawa zake kuwaelekea Idris na Merice na kusababisha mlipuko mkubwa na wa haja.


“Tutokeni humu haraka sana.”Uzo aliongea na kuanza kujikusanya tayari kwa kutoka ndani ya maabara ambapo kulikuwa kumechafuka kwa mapambano aliyoyaanzisha Unknown. “Jenero, tutoke.” Akabwata baada ya kumuona Jenero akiwa anatizama ile filamu ya kumpendeza machoni mwake na wakati huo, ile roketi ilijibadili tena na kuwa roboti kisha kutua chini mbele ya Merice na Idris ambao walikuwa wameyapangua yale mabomu kwa kuyapiga pembeni na kulipuka huko. Lakini wakati wanaweka akili zao sawa, ndipo wakashtukia, The Lens yupo usoni mwao kujikuta wanapokea makofi mazito yaliyowatupa pembeni kabisa ya maabara ile.


“Hii ndio silaha ambayo nataka kuijenga. Inavutia sana tena sana. Hili wazo tungelipata sisi, tungetisha sana.” Jenero alijiongelea baada ya kuona mbwembwe za The Lens ambaye alikuwa anatoa mambo ya kushtukiza {surprise} kwa wakina Idris.


“Tutoke humu Jenero.” Uzo aliongea na kuanza kumvuta Jenero ili watoke nje.


“Unadhani nani atashinda hii vita?” Jenero akauliza wakati Uzo anamvutia kwenye mlango wa kutokea.


“Jenero twende zetu. Humu si pazuri tena.” Uzo akasisitiza na wakati huo wanajeshi wanamichezo walikuwa mlangoni wakisubiri wakuu wao wapite ndipo nao watoke.


“Hao makemikali wenu, hata waje mia, hawawezi kushinda hiyo zana hapo. Ina kila silaha na kila mbinu zinazohitajika kwenye mapambano.” Jenero akawa anazidi kuongea lakini safari hii tayari alikuwa ametolewa kwenye kile chumba na kubakiza mashine za vita zikipambana.


Idris akainuka tena kama mzimu na mkono wake ukageuka kuwa silaha nzito ambayo ilianza kumtupia The Lens mabomu lakini Unknown ambaye ndiye alikuwa anaendesha lile roboti, alikuwa anayekwepa na kuyapangua yale mabomu kwa ustadi mkubwa na Idris akajikuta anaacha kwanza kumaliza silaha zake bila sababu ya msingi.


“Ndicho ulichobarikiwa kuwa nacho we’ nguruwe mweusi?” The Lens, akamuuliza Idris.


“Hapana. Sina hiyo tu. Nina hii pia.” Idris akaongea na hapohapo akabadilika na kuwa mwekundu sana kama moto mkali unaowaka kwenye msitu mkubwa uliokauka miti yake. Idris akapiga chini kwa mikono yake miwili, mlipuko mkubwa ukatokea eneo lile huku The Lens akirushwa vibaya sana na kutolewa nje kupitia kule dirishani.


Kila alipotaka kujibadilisha na kuwa roketi, ilishindikana na alikuwa anashuka chini kwa kasi ya ajabu sana. Alijaribu tena na tena, lakini ilishindikana na tayari alibakiza sekunde ndogo sana kufika chini. Ndipo alifanya maamuzi ya kuacha mwili wa The Lens na yeye kwa kutumia viatu vyake, akachomoka mle ndani na kupaa juu alipotoka, huku mwili wa The Lens ukijibamiza chini na kusababisha mshindo mkuwa sana eneo lile.


Unknown akarudi kulekule alipotoka na alipoingia tu, akakutana uso kwa uso na Idris ambaye alirusha ngumi moja kali, lakini Unknown aliiona na kuegama kidogo upande mwingine, ngumi ikapitiliza na wakati huo naye Unknown akirusha ngumi yake na kumpiga kisogoni Idris ambaye badala ya kugugumia maumivu, akamtazama Agent kwa macho ya kumsikitikia.


“Usiniangalie kimahaba hapa. Mimi siyo hao wajinga wenzako.” Unknown aliongea kwa kujinadi huku akiingalia saa yake ambayo ndio iliendesha mwili wa The Lens.

Ilionesha kuwa nguvu za roboti yule zilikwisha baada ya kukutana na nguvu zingine za jua kutoka kwenye mwili wa Idris. Na sasa, saa ile ilionyesha kuwa, nguvu imefikia asilimia ishirini ili ijirudi tena upya. “Nitakuua wewe, na kisha nitaenda kuwaua wanajeshi wenzako wanaojifanya wanajua sana kucheza na mipira.” Akaongezea kwenye kauli yake ya mwanzo lakini yote hiyo ilikuwa ni kupoteza muda ili roboti wake arudiwe na nguvu. Alijua wazi kumpiga Idris ni ndoto za kuota unakufa.


“Sina bosi. Na ninakuua leo.” Idris alimjibu Unknown na kuruhusu mkono wake kutoa bunduki ndogo aina ya uzi, na kuanza kumshambulia Unknown ambaye alikuwa anakimbia na wakati huo risasi zikiwa zinamkosa kosa kumpata.

Idris akabadilisha bunduki na kutoa bunduki ambayo ilikuwa na uwezo wa kutoa mabomu na risasi kwa pamoja kama utaruhusu.


Bunduki ile ilianza kutema risasi zake kwa wingi sana Agent alipoona hali imekuwa tete, akajificha nyuma ya jokofu moja ambalo lilikuwa limetupwa pembeni. Akiwa kajificha hapo, alijua hamna risasi ambayo itaweza kutoboa jokofu, ila kuna njia moja pekee ya kuweza kumfikia pale.

Akachomoa bunduki yake ambayo ilikuwa inaning’inia kwapani. Kisha akaifungua na kuiweka sawa tayari kwa uvamizi na wakati huohuo, alisikia bunduki ya Idris ikiwekwa sawa upande wa mabomu. Unknown akajilaza kitumbotumbo na bunduki yake akaielekezea upande mwingine kwa sababu upande wa mbele ulikuwa una jokofu.


Sauti ya kutoka bomu ikasikika kwenye bunduki ya Idris, na bomu hilo lilienda kutua kwenye jokofu, kisha likanyanyua lile jokofu kwenda juu, na kulitupia mbali kabisa na pale alipokuwa kalala Agent Unknown. Na wakati jokofu hilo likinyanyuliwa, Unknown yeye hakuwa na haja nalo na aliachana nalo kabisa. Alirudisha bunduki yake mbele toka kule pembeni na kuweka jicho lake kwenye lens. Akamuona vema Idris akiwa na bunduki yake tayari kwa kuanza tena mashambulizi.


Agent Unknown, akaachia risasi moja na kumkuta Idris kifuani. Akaikoki tena na kumpiga tena palepale na kumfanya Idris arudi nyuma kwa sababu ya misukumo ya risasi zile. Unknown akaikoki tena na kumlenga Idris kwenye kichwa chake lakini ghafla alijikuta akiiachia bunduki yake na kulia kwa maumivu sana. Kisu kidogo kilizama kwenye mkono wake na alipotazama ni nani kafanya yale, alimuona Merice ambaye alianza kujizoa zoa na kuinuka tangu muda ule alipozabwa kofi na The Lens.


Unknown akaanza kukimbilia mlangoni walipotokea Uzo na wenzake huku akivua kata mikono yake na kisha kukichomoa kile kisu na kukitupa pembeni. Akatumia ile fulana yake ya kata mikono kwa kufunga jeraha ambalo alilipata muda ule huku akiwa kajificha nyuma ya mlango. Akatazama saa inayoonyesha nguvu za The Lens, ikawa imeandika asilimia tisini na tano na inaelekea kuwa tisini na sita. Kisha akachungulia kule walipo maadui zake. Akashuhudia Idris akijiminya na kuchomoa zile risasi mbili na matobo yaliyopita risasi zile, yakijifunga na kurudi katika hali ya kawaida.


“Pumbavu hawa. Sijui wanatengeneza majitu ya hivi ya nini,” Agent alijiuliza huku akiwa kaacha kumchungulia Idris. “Zile risasi zilitakiwa zimpige na kumtokea mgongoni. Ila zilibaki mwilini mwake. Sasa kumbe ni liroboti tu nalo hili.” Akamaliza kwa tusi.

Akachomoza uso wake tena na kuchungulia na alishuhudia macho ya Idris yanatoa mwanga wa kijani ambao ulikuwa unapanda na kushuka toka kwenye chumba kile.






“Pumbavu hawa. Sijui wanatengeneza majitu ya hivi ya nini,” Agent alijiuliza huku akiwa kaacha kumchungulia Idris. “Zile risasi zilitakiwa zimpige na kumtokea mgongoni. Ila zilibaki mwilini mwake. Sasa kumbe ni liroboti tu nalo hili.” Akamaliza na tusi.

Akachomoza uso wake tena na kuchungulia na alishuhudia macho ya Idris yatoa mwanga wa kijani ambao ulikuwa unapanda na kushuka toka kwenye chumba kile.

“Mbwa ananitafuta huyu,” Akaongea Unknowm ma kutizama saa yake. Ikawa ipo asilimia tisini na tano. Akachungulia tena lakini eneo lile, hakumuona Idris. Akarudisha kichwa ndani na hapohapo, akashangaa Idris ametokeza mbele yake na kumkaba shingoni na kisha kuanza kumnyanyua juu kwa kutumia mkono mmoja. Miguu ya Unknown ikawa inaelea, na huku juu akawa anajaribu kuindoa mkono wa Idris shingoni kwake lakini mwanaume hakumuachia.


Mkono mwingine wa Idris, ukachomoa panga refu na wakati huohuo, saa ya Agent Unknown ililia sauti ambayo iliashiria, nguvu za roboti wake, tayari zilirudi hadi asilimia mia. Agent akajitahidi kuupeleka mkono wake mwingine kwenye saa yake na kisha akaibonyeza saa ile kwenye kitufe kimoja kilichokuwepo pembeni.

Idris naye alikwisha dhamiria kummaliza kabisa Unknown. Aliuvuta mkono wake wenye panga kwa nyuma, tayari kwa kumshindilia kichwani panga lile Unknown.


Lakini kabla hajatimiza adhma hiyo. Mkono wa The Lens ulitokea na kuingia kwenye mkono wa Unknown na Agent hakufanya kosa hata kidogo. Alitumia mkono ule wa chuma kwa kumtwanga konde zito Idris. Konde hilo lilitua kwenye kidevu na kumfanya Idris amuachie Unknown huku kidonda kikubwa kikijitengeza kwenye kidevu.


Vile vifaa vya The Lens vikarudi na kujitengeneza tena na kuwa roboti kubwa sana. Unknown akafungulia viatu vyake, naye akapaa na kuingia mwilini mwa The Lens ambapo yeye alikaa kwenye kiti kimoja ambacho kilikuwa kifuani kwa roboti yule.


“Muda wangu sasa. Mmenionea sana.” Unknown aliongea kwa kisirani na kuubadilisha mwili wa The Lens kuwa kioo kwa asilimia kubwa sana.


Nyuma ya The Lens, alikuwepo mwanadada Merice ambaye alijichaji nguvu zake nyingi nakuzirusha kwenda kwa The Lens. Lakini hakujua sababu ya The Lens kujigeuza kuwa kioo. Mwili ule ulijengwa kwa kioo ili aukisi kila nguvu ya jua au moto kila utakapovamiwa. Na kosa kubwa alilofanya Merice, ni kurusha nguvu hizo za jua {nyuklia} kwenda kwa roboti yule ambapo nguvu zile zilidunda na kumrudia yeye mwenyewe na kumpiga vibaya sana kwa mlipuko uliyojitokeza.


Idris aliweza kushuhudia tukio like na kujikuta akikumbwa na maumivu yaliyochanganyika na hasira. Hali hiyo ilimfanya naye aanze kupigana bila huruma na wakati huo, kidevu chake kilikuwa kimejirudi baada ya kupokea konde zito la chuma toka kwa Unknown.


Idris akapotea pale alipo na ghafla akatokea mbele ya The Lens na kuanza kutumia kisu kuchimbua miguu ili kukata nyaya zilizoungwa kwenye mwili wa The Lens. Macho yake yawezayo kuona hadi ndani, yaliweza kugundua uwepo wa nyaya zinazomuendesha The Lens hivyo alianza kuchimbua mwili wa The Lens ili aziharibu.


The Lens alitupa teke lililompata Idris tumboni na kumrusha toka mahali alipo na kwenda kujibamiza kwenye ukuta na wakati huohuo, The Lens naye aliruka juu kidogo na kisha kutua mbele ya Idris tena na kumshindilia ngumi nyingine akiwa palepale chini. Idris alipotaka kupotea kama afanyavyo, alijikuta anaumia mwenyewe. Vile vioo vya The Lens viliakisi nguvu zake na kujikuta hawezi kupotea bali kubaki palepale na kupokea kipondo cha nguvu. Alipotaka kutengeneza nguvu za nyuklia, akakumbuka hali iliyomtokea Merice. Uoga ukamkumba. Angejilipua yeye mwenyewe, lakini aliona ni mapema sana hasa kwa sababu hajawamaliza maadui zake.


“Umeshindwa mwanajeshi. Sasa ni muda wa kufa.” The Lens alimwambia Idris.


“We’ ni nani?” Ikabidi Idris amuulize The Lens hasa kwa kile kichapo alichokipokea.


“The Lens.” Ilikuwa ni sauti nene iliyomjibu Idris.


“Hapana. Nataka kukujua wewe unayeendesha hii silaha.”


“Kwa kuwa upo katika wakati wako wa mwisho, naweza kukwambia,” Akajibiwa Idris na kujiweka tayari kumjua anayempa kashi kashi. “Naitwa The Last, kwetu Tanzania naitwa Wa….” Hakumaliza kauli yake, Idris akadakia.


“Wa Mwisho. Au Man’Sai. Baba Martina, mume wa Lisa.” Kauli hiyo ikamfanya The Lens kutulia kidogo na kisha Agent Unknown akachomoka toka mle ndani na kushuka hadi chini alipokuwepo Idris.


“Umenijuaje?”


“Nina urafiki na Watanzania. Nimeishi kule na nimeoa kule. Nina urafiki ambao si mkubwa sana na Agent Zero. Ndiye aliyenijenga na kufika hatua ya kupambana hivi.” Akajibu Idris.


“Agent Zero,” The Last alinong’ona. Idris akaitikia kuwa anajuana naye. “Ni mwanafunzi wangu yule.” Akaongeza The Last.


“Nafahamu na tulifika hadi FISSA, mimi na Merice na kuonana na uongozi wako. Kwa kifupi, wamekukumbuka sana.” Maneno hayo yakamfanya The Last apumue pumzi kubwa na kukumbuka mara ya mwisho alipotizama runinga. Alikumbuka kuwa Merice na Idris ndio walikuwa wamekamatwa na jeshi la Uzo.


“Sasa imekuwaje mkataka kutengenezwa tena humu?” Akauliza The Last.


“Hapana. Walitaka kutuua. Yaani damu yangu, watengenezwe wanajeshi wengine wenye roho mbaya kupitia mimi. Lakini mimi na Merice tulikwishapanga kuhusu hilo. Nilitaka na Merice awe kama mimi, na wa kutubadilisha alikuwa ni mama yake. Agent Zero alisoma njia karibu zote za kumbadilisha Merice, lakini mitambo ya kufanya hivyo, haikuwepo kule Tanzania. Ndipo akachukua jukumu la kumtumia barua pepe Mama wa Merice kumuonyesha njia ya kutengeneza wanajeshi wengine kama mimi. Hakujua ile barua kuwa imetoka kwetu. Naye akaongeza kazi ya kutuhitaji ili atufanyie huo ujinga. Hakujua kuwa ananipa nguvu zaidi.” Idris akaeleza kwa kifupi kilichotokea.


“Wajua nini. Hatuna muda sana wa kuongea. Nina watafuta wale wajinga wanamichezo nimalizane nao. Naomba nikawafanye kitoweo. Samahani sana kwa kilichotokea.” The Last aliongea na kuwasha viatu vyake tayari kupanda ndani ya The Lens.


“Namuhitaji Uzo pia. Anahusika na kifo cha wazazi wangu. Nahitaji alipe yote aliyoyafanya.” Idris alimwambia The Last.


“Unahitaji Lift?” Maneno hayo yalienda sambamba na The Lens kubadilisha vioo na kuwa ile Roketi. Idris akanyanyuka na kwenda kupanda nyuma ya The Last ambaye alikuwa ndiye dereva.


Roketi ikawashwa na kuanza kwenda kwenye lile dirisha ambapo The Lens alitupwa na mlipuko alioutoa Idris. “Hey. Unaweza kukaa na mwenzako huko nyuma?” Akaulizwa Merice ambaye alikuwa bado hajarudiwa na nguvu baada ya ule mlipuko uliyojirudi kwake.

Merice akamtazama Idris, akamuona asiye na wasiwasi.


“Id. Ni nani huyu?” Ikabidi naye aulize swali lilelile kama aliloulizwa The Last baada ya kichapo kikali kumuangukia.


“Ndiye The Last.” Akajibiwa kwa kifupi.


“Man’Sai?” Akauliza kwa mshangao wa haja.


“Hatuna muda dada. Tupande, tukamalize kazi.” The Last aliongea na Merice bila kuuliza tena, akapanda nyuma na kumkalia juu Idris. Roketi ile ikachomoka toka mle ndani na kuanza kwenda nje umbali kama kilomita mbili.


“Hatuhitaji tena huu ujinga. C.O.D.EX, ndio mwisho wake.” The Last aliongea huku anafungua vifuniko kwenye vifyatulio vya mabomu yaliyopo kwenye mabawa ya ile roketi. Akatuma bomu moja ambalo lilienda hadi kwenye ile maabara kuilipua vibaya sana.


Mlipuko ule ulifanya waliokuwepo chini pia washtuke hasa baada ya ghorofa lile kuwa kivutio kikubwa sana Jijini New York. Maabara ya C.O.D.EX ikawa imelipuliwa. The Last akaishusha roketi ile hadi chini, mbele ya jeshi jipya lililoitwa na Jenero, F.O.F. Roketi ikajibadilisha na kuwa The Lens huku Idris na Merice wakitokea na kusimama pembeni ya roboti yule.

ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog