Search This Blog

Thursday 29 December 2022

KIGUU NA NJIA - 4

 

  Simulizi : Kiguu Na Njia

Sehemu Ya Nne (4)


“Mnakwenda wapi?” Dereva aliniuliza.


Sikuwa na pa kwenda. Nilichohitaji ni kuondoka eneo hilo kuelekea popote. Sikuwa tayari kuwaona wale vijana wa Kimasai tena. Kwani kama wasingeniua mimi ningewaua wao au mmoja wao.


Pia sikuwa tayari kutazamana na akina Leakey macho kwa macho, iwapo wangerejea ghafla kutokana na hasara niliyowatia.


“Wapi?” Dereva alihimiza.




“Kwani nyie mnakwenda wapi?”

“Singida, kupitia Babati,” Sikuhitaji kumjibu. Niliparamia gari lake. Msichana alifanya hivyohivyo. Tukaondoka. Tulipumzika kwa muda. Nilitumia mapumziko hayo kumvuta kando na kumtaka abakie hapo na kuwatafuta ndugu zake wengine. Alikataa katakata kwa maelezo kuwa toka alipokataa tohara tayari amekataa ndugu wote hivyo hana mahala pa kwenda.

“Kwan nini usikubali kupata tohara?” Nilimhoji. “Naogopa.” Lilikuwa jibu lake.

“Unaogopa?”

“Kufa. Mwenzangu alikufa jusi tu.” Alisisitiza.

“Lakini mimi sina pa kukupeleka. Mwenyewe sijui nitakwenda wapi, nitalala wapi. Huoni kuwa unanipa mzigo juu ya mzigo?” Nilijaribu kumshawishi. Badala ya kunielewa aliangua kilio. Kwa mara nyingine ushujaa ulinitoka, ubinadamu ukachukua mkondo wake.

Kwa bahati nzuri nilikuwa na tabia ya kutembea na akiba yangu yote ya fedha mfukoni, isipokuwa zile zilizokuwa benki peke yake. Hivyo, mkasa huo ulinikuta nikiwa na vijisenti ambavyo vingeweza kuniweka hai kwa wiki mbili tatu kabla ya kuanza kutaabika kwa njaa. Nilitumia sehemu ya senti hizo kulipia nauli na kula chakula cha mchana kabla ya kuanza tena safari ya Singinda.

Mzee mmoja tuliyekuwa naye safarini humo. Nadhani alisoma sura yangu iliyojaa mashaka na ule uso wa Kimasai uliolowa machozi. Aliniuliza kulikoni. Nilihitaji sana ushauri hivyo sikusita kumsimulia kila kitu, toka mwanzo hadi mwisho wa mkasa. Kwa mshangao wangu nilimwona akiangua kicheko baada ya kunipa pole.




“Sioni kama kuna jambo la kuchekesha hapo,” nilimwambia kwa sauti ndogo iliyoficha hasira zangu dhidi ya kitendo chake hicho.

Mzee alinishika bega kabla ya kuninong’oneza ili msichana yule asisikie. “Nacheka kwa kuwa unasumbuliwa na jambo dogo sana,” alinieleza.

Sikumwelewa. “Dogo kivipi? Mtoto wa watu hana pa kwenda kwa sababu ya uzembe wangu. Mimi mwenyewe sina pa kwenda kwa sababu ya uzembe uleule. Unaliita jambo dogo?” nilimwuliza.

“Dogo sana.” Alisema. “Nitakusaidia mara tutakapofika Singida. Naitwa Kingu. Halfan Kingu. Kwa hilo ondoa wasiwasi mwanangu.”

Nilishusha pumzi. Kwa muda nilisahau matatizo yangu na kuifurahia safari kwa kuyaruhusu macho yangu kuburudishwa na mandhari mbalimbali za mazingira kando mwa barabara hiyo. Mbuga pana zilizojaa ndege na wanyama ainaaina zilitulaki, majabali yaliyosimama katika maumbile ya kusisimua yalitushangaza, majangwa yasiyo na msitu wala nyasi nayo yalikuwa sehemu ya mazingira hayo.

Tulifika Singida jioni sana. Wakati huo tayari roho yangu ikiimba tenzi na mashahiri juu ya Singida niliyoifahamu kupitia simulizi za kihistoria na maandishi ya vitabuni.

Kwa mfano, nilipata kusoma juu ya reli iliyojengwa enzi za vita kuu inayounganisha mji huo na reli ya kati kupitia Manyoni. Leo nilikuwa nimepata fursa ya kuiona kwa macho yangu mwenyewe reli hiyo.

Singida, nchi ya mwanamke pekee shujaa katika historia ya mapambano ya Watanganyika dhidi ya ujio wa wakoloni. Mwanamke huyu Leti Kidanka, kati ya mwaka 1903






hadi 1907 aliongoza majeshi ya Wanyaturu kupambana na yale ya Wajerumani hata wakaelekea kusalimu amri. Kama isingekuwa kwa ajili ya silaha zao kali na nyingi Wajerumani wale wasingefanikiwa kumkamata, wakamchinja na kuondoka na kichwa chake kama walivyofanya kwa Mkwawa.


Niliweza kuyaona majengo ya kale, boma la kilimatinde walilojenga Wajerumani hao kati ya mwaka 1880 na 1890 na lile la mkoloni lililojengwa 1900 hadi 1911. Boma ambalo lilikuwa makao makuu, ofisi, gereza, makazi ya maafisa wao na eneo la kunyongea watu. Nilishangaa kuona mti uliokuwa ukitumika kunyongea watu toka enzi zile ukiwa hai hadi leo.


Mzee Kingu ambaye tulifuatana naye katika safari hiyo ya mjini baada ya kuhusika kwenye gari alitabasamu kila aliponiona nikivutiwa na hiki au kile.


“Laiti ungefika Iramba,” alisema na kuongeza “Kuna vivutio tele ambavyo kwa udadisi wako vingekusisimua sana. Kuna mapango kama yale ya Kondoa Irangi na majabali yaliyoumbwa kwa namna ya binadamu,” alisema.


“Unaifahamu Sodoma na Gomora?” Aliniuliza ghafla. “Naam. Imesimuliwa katika Biblia na Koran,” nilimjibu. “Unafahamu chochote juu ya mwanamke aliyegeuka


mwamba wa chumvi baada ya kugeuka nyuma kuutazama mji wa Sodoma ukiteketea kinyume cha maelekezo waliyopewa?”


Hili pia nililifahamu, “Mke wa Lutu sio?”


Mzee Kingu alitikisa kichwa kuafikiana nami. “Kwa taarifa yako sanamu ya mwanamke yule aliyeganda na kugeuka nguzo ya chumvi iko huku kwetu. Ukienda Iramba, uingie maporini utaikuta. Na chumvi inapatikana hadi leo kama ilivyoandikwa,” aliongeza.


“Wewe ulipata kuiona?” Nilimuuliza.



“Sijapata lakini wazazi wangu walinihakikishia. Wao walikuwa wakienda huko katika safari zao za uwindaji.”

Sikuweza kumkubalia wala kumkatalia. Tulikuwa tukitembea mjini. Yeye mbele, mimi kati, msichana wa Kimasai nyuma. Ilikuwa safari iliyobuniwa na mzee huyo kwa maelekezo kuwa ni ya kunisaidia. Hata hivyo, alikuwa hajaniambia tunakwenda wapi.

Vivutio vya mji wa Singida havikuwa na mwisho. Maziwa yaliyojikita katikati ya mji, Singidani na Kindai ni miongoni mwa mambo ambayo yasingekosa kumvutia mgeni yeyote. Sehemu fulani tuliwaona wavuzi wakitafuta riziki zao katika maziwa hayo, huku ndege kama bata maji na yangeyange nao wakijishughulisha na yao.

Safari yetu iliishia mbele ya jengo moja lililokuwa na maandishi yaliyosomeka EVANGELICAL LUTHERAN AUGUSTANA SYNOD. Kingu aliniambia kuwa hiki kilikuwa kitengo cha kanisa ambacho kilijishughulisha na kusomesha watoto yatima na wale wasiojiweza. Aliniambia kuwa wasingesita kumpokea msichana huyo na kumlea, hasa baada ya kuonyesha msimamo wake wa kupingana na mila potofu za jamii yake.

Nilimweleza hivyo msichana yule. Nilishukuru kuona akiipokea habari hiyo kwa utulivu. Tulikaribishwa ndani. Mtumishi aliyetupokea hakushangazwa na maelezo yetu hata kidogo. Alimshika msichana yule mkono kwa dalili zote za upendo kabla ya kumwuliza umri wake.

Hakujua ana miaka mingapi. Kwa kukadiria kwangu hakuzidi miaka kumi na miwili. Mchungaji wao hakuwepo. Hivyo alitutaka mimi na Kingu kuondoka kwa maelezo kuwa msichana huyo alikuwa katika mikono salama.




Tuliinuka. Nilishangaa kuona msichana huyo naye akiinuka na kunifuata. Nilimtazama kwa macho makali yenye maswali mia moja na moja. Hata hivyo, nilipumua pale nilipomuona akitabasamu na kisha kusema kwa kiswahili chake kibovu, “Taka kushukuru. Yenyewe imeokoa maisha yangu.”

Alinikumbatia. Machozi yakimlengalenga machoni.

Kitendo chake kiligusa ile sehemu laini katika moyo wangu. Mie pia nilihisi machozi yakinilengalenga. “Hapana ni wewe uliyeokoa maisha yangu,” nilimwambia. Ulikuwa ukweli toka katikati ya moyo wangu.

“Hapana kweli… mimi haribu maisha yako,” alijitetea.

Sikutaka kuendelea na mjadala huo. Hivyo nilijikwanyua taratibu toka katika mikono yake na kuanza kuondoka, huku nikijitahidi kuyaepuka macho yake.

Hutaki kujua hata jina langu? Nilihisi swali hili katika macho yake. Nikajikuta nikitokwa na swali hilo.

“Mimi naitwa Nashifa,” alisema.

“Vizuri sana Nashifa. Mimi naitwa Petro. Petro Kionambali,”


* * *

Kuutua ‘mzigo’ ilikuwa mwisho wa tatizo moja. Tatizo la pili, langu binafsi lilikuwa palepale. Sikujua usiku huo na siku zinazofuata ningekitua wapi kichwa changu wakati nikianza upya kufikiria hatma ya maisha yangu, baada ya miaka kadhaa ya kuzungukwa na akina Leakey katika Bonde la Ufa na miji au vijiji vya jirani.

Nadhani kwa mara nyingine Kingu aliweza kuusoma moyo wangu. Ni pale nilipomsikia akianza kujinadi ghafa






kwamba anatoka katika ukoo unaoheshimika na usio na njaa. “Wanyaturu wote wananifahamu. Natoka katika ukoo wa Machifu. Huyu unayemsikia Chifu Said Gwao mdogo wangu upande wa baba. Kwangu utalala, utakula bila wasiwasi wowote.”


Nikashtuka. “Hayo yametokea wapi tena?” nilimwuliza.


“Naona unasumbua kichwa chako kufikiri leo utalala wapi,” alinijibu. “Hilo achana nalo kabisa mwanangu. Fikiria mengine.”


Nilimtumbulia macho ya mshangao uliochanganyika na aibu. “Nisingependa kukusumbua zaidi. Tayari umenisaidia sana. Kunipatia makazi ya yule msichana lilikuwa tatizo langu kubwa. Mengine sioni kama yatanisumbua,” nilimweleza.


“Huwezi kulala nje. Huwezi kutupa pesa katika vyumba vya wageni kwa ajili ya kulala tu. Utakuwa mgeni wangu. Leo, kesho na keshokutwa. Utakaa hadi hapo utakapoamua vinginevyo.”


Sauti yake iliashiria kufunga mjadala. Akiwa mtu mwenye umri mkubwa, bila shaka zaidi ya baba yangu, ingawa hakumpata babu, nililazimika kumsikiliza. Tukaongozana kuelekea kwake. Yeye mbele mimi nyuma.


Mzee Kingu alikuwa akiishi nje kidogo ya mji. Kauli yake kuwa hakuwa mtu mwenye njaa ilidhihirika mara tulipofika nyumbani kwake. Kwa kweli haikuwa nyumba bali majumba. Alikuwa na kijiji! Nyumba kama nane hivi, zikiwa katikati ya shamba la ekari zipatazo tano au zaidi, za matama na alizeti. Tatu zilikuwa nyumba za wake zake, nne za wanawe na moja niliyoambiwa kuwa ilikuwa maalumu kwa ajili ya wageni. Pembeni alikuwa na zizi kubwa la mifugo. Milio ya ng’ombe na mbuzi ilisikika.



Tofauti na alivyokuwa safarini, mcheshi na mzungumzaji sana, hapa nyumbani alikuwa mtu mwingine kabisa. Tulifika yapata saa mbili za usiku. Mji huo ulikuwa umechangamka kwa kelele za watoto, sauti za redio na pilikapilika za akina mama. Hali ambayo ilibadilika mara mzee alipotia mguu katika himaya hiyo. Wajukuu walipunguza kelele, kila mmoja akirejea kwa mama yake. Watoto walimfuata na kumsalimu, lakini katika hali ambayo haikuwa tofauti sana na salamu za askari na afande wake. Walibadilishana maneno mawili matatu, ya juujuu, kabla ya watoto hao kuteleza kila mtu akienda anakokufahamu. Hali haikuwa tofauti sana na wake zake wadogo. Ni mke mkubwa pekee ambaye baada ya kumsalimu aliketi na kumwuliza habari za safari. Hata hivyo, baada ya dakika moja tu yeye pia alijikuta hana cha kuzungumza. Aliketi pale kwa utulivu kama anayesubiri amri, ambazo zilianza kumiminika mara moja.

“Huyu ni mgeni wangu. Chumba chake kimeandaliwa?” “Wale ng’ombe wawili wagonjwa wamepatiwa dawa?” “Nina mashaka kama mmekumbuka kurekebisha lile

ghala linalovuja…”

Mkewe ambaye tayari alikuwa mama wa makamo alijibu kila swali kwa ufupi na umakini mkubwa kama mwanafunzi kwa mwalimu wake.

Muda mfupi baadaye chakula kililetwa. Hakikuwa chakula cha watu wawili wala watatu. Ulikuwa mlo ambao watu sita wangeweza kula na kusaza. Ulikuwepo mguu wa mbuzi wa kuchoma, kuku wawili waliopikwa, sinia kubwa la wali na bakuli la matunda. Wakati mimi niliishia kula mapaja mawili ya kuku na wali kidogo mzee Kingu aliteketeza robo tatu ya chakula kile. Alikula nusu ya matunda na kushushia kwa birika zima la maji.




“Endelea kula.” Alinihimiza “Mimi nimechoka. Unajua utu uzima tena! Watakuonyesha sehemu ya kulala,” alisema akiondoka bila kusubiri shukrani zangu.

Mie pia uchovu ulikuwa umenishika. Hivyo, mara alipoondoka nilinawa mikono, nikamshukuru bi mkubwa ambaye muda wote alikuwa pale. Kisha niliomba nielekezwe yalipo malazi yangu. Mvulana mmoja alinipeleka kwenye nyumba ya wageni. kiasi ilijitenga na nyumba nyingine na hivyo kutoa uhuru wa kutosha kwa wageni. Taa ya chemli ilikuwa ikiwaka chumbani, kando ya kitanda kilichotandikwa kwa blanketi na shuka mbili safi. Mara tu kijana huyo alipotoka nilivua nguo zangu na nikafunga mlango na kisha kujibwaga kitandani.

Mkesha wa siku hiyo, uchovu wa safari ya miguu na gari pamoja na purukushani za siku nzima vilifanya usingizi unichukue mara tu nilipokitua kichwa changu juu ya mto. Ulikuwa usingizi wa pono. Nililala hadi saa tisa au kumi za alfajiri nilipoamshwa na kitu fulani. Sikufahamu ni kitu gani lakini hisia zilifanya nishuku jambo. Sina tabia ya kukoroma, bado niliamini kuwa nilijisikia kama nakoroma usingizini. Nilitulia kimya nikijaribu kufikiri kitu gani kiliniamsha. Sikuelewa. Wakati usingizi ukianza tena kunichukua hisia zilezile za kukoroma zilinireja. Hapa, hazikuwa hisia. Ilikuwa sauti halisi ya kukoroma tena ikitoka chini ya kitanda.

Nilishuka toka kitandani, nikapandisha mwanga wa taa na kuchungulia uvunguni. Nilishangaa kuona kitu kama tochi mbili zikinimulika toka chumbani humo. Tukio ambalo lilifuatiwa na mguno mzito kama ule wa mbwa anayehisi kuhatarishiwa uhai wake.

“Fisi!”




Niliropoka baada ya kutazama vizuri. Fisi mkubwa kabisa alikuwa amelala uvunguni humo, chini ya kitanda changu! Nilitetemeka. Nikaruka kuendea nguo zangu ambazo nilivaa harakaharaka na kutoka mbio.

Mbio ambazo ziliishia mbele ya nyumba ambamo nilimuona mzee Kingu akiingia kulala. Kabla hata sijagonga niliona mlango ukifunguliwa, mzee akiwa amevaa kikoi, kifua wazi. Alitoka. “Kuna nini?” alihoji kwa sauti kali kidogo.

“Fisi yuko chumbani kwangu.” Nilimjibu.

Mzee akaangua kicheko. “Hilo tu?” alinihoji baadaye. “Yule pale hana neno. Zaidi anakulinda kama anavyoulinda mji huu.”

Sikumwelewa. “Hana madhara! Kwa hiyo nikalale na


fisi?”


Mzee alicheka tena. Kisha akasema, “Kumbe wewe bado


mtoto mdogo sana sio? Unadhani himaya hii utailinda vipi bila kuwa na vitu kama vile? Yule amefugwa. Anatii amri zangu zote na hafanyi jambo lolote bila maagizo yangu. Isitoshe ni mtumishi mzuri anayebeba mzigo na hata kunibeba mimi mwenyewe katika safari zangu za usiku.”

Nilizidi kuchanganyikiwa. Nazungumza na binadamu au shetani? Anazungumzia kufuga fisi kama kufuga mbwa!

“Binadamu anawezaje kumfuga mnyama kama yule?” nilimwuliza bila kutarajia.

Na bila kutarajia vilevile alinijibu. “Ujuzi tu mdogo wangu. Nyie mnaita uchawi lakini ni ujuzi. Ukipata jino la fisi unaweza kumfuga fisi. Ukipata la mamba unaweza kummiliki mamba. Vivo hivyo kwa simba, chui na hata nyoka. Watu wanawafuga binadamu wenzao washindwe kumfuga mnyama?” alisema. Sasa nilikuwa na hakika kuwa sizungumzi na binadamu





wa kawaida. Sikuona kama nilihitaji kuendelea kumsikiliza. Alizisoma hisia zangu. “Nenda kalale,”akaniamuru.

Nikageuka kuondoka. Mara akaniita tena, “Kijana,” alisema. “Kitu kimoja kinanisumbua. Umekula nini wewe?”

“Nimekula nini? Una maana gani?” sikumwelewa.

Maana wenzako wote hulala na fisi wangu hata kwa

mwezi bila kumwona wala kumsikia. Wewe umetafuna nini?”

Sikumjibu. Niliondoka. Wala sikurudi kwenye banda lake la kuchangia na fisi. Nilipitiliza kuifuata njia iliyonifikisha katika mji huo. Nilitembea taratibu hadi mjini. Alfajiri ilinikuta nikipitapita katika mitaa ya mji huo. Jua lilipochomoza lilinikuta nimeketi kando ya ziwa Singidani nikitazama pilikapilika za wavuvi.

Sikuwa na wazo jingine zaidi ya kutafuta gari litakalonipeleka kokote kwenye usalama. Sikuwa tena na hamu ya kuendelea kuivinjari Singida.

Niliuliza mahala wanapopandia magari ya kwenda mikoani, nikaonyeshwa. Sikusita kulipia nauli ya kwenda Kilimanjaro na kuianza safari mara moja.


?

17

Ben R. Mtobwa












SURA YA KUMI NA SABA?

Kilimanjaro, Paa la



N

ilikuwa nimesikia mengi ju ya Kilimanjaro, mlima mrefu kuliko wote barani Afrika. Hali kadhalika, nilisoma mengi na kutazama picha nyingi

zilizoonyesha mlima huo. Lakini katika yote hayo niliyosikia au kuona kwenye picha hakukuwepo lolote lililoniacha nisiweze kupigwa na butwaa huku nikiwa siyaamini macho yangu pale nilipoutia machoni mlima huu. Kwa kweli, ni mlima ambao lazima uuone, kusimuliwa pekee kulikuwa hakutoshi.

Ilikuwa ndio kwanza nashuka toka katika basi lililonileta mjini hapo, macho yangu yalipopokelewa na utukufu ule. Ujio wangu Kilimanjaro ukiwa umefanyika bila matarajio baada ya yale mapokezi ya kutisha niliyoyapata Singida. Mapokezi ya kulazwa chumba kimoja na fisi.

Ni mawazo hayo yaliyofanya Singida kama nuksi nyingine iliyokuwa ikinisubiri. Hali iliyopelekea baada ya siku mbili tatu za kuzurula mjini hapo nipande basi lililonileta Kilimanjaro, kwa matarajio ya kupata kazi au biashara yoyote ambayo ingeniwezesha kupata chochote ili nitimize azma yangu ya kurudi nyumbani. Azma ambayo umuhimu wake uliongezeka siku baada ya siku.

Mlima ulisimama pale kwa kiburi na fahari zote. Ulikuwa?




peke yake, ukiwa umechomoza hadi juu ya mawingu, kiasi cha kujionyesha vizuri popote uliposimama katika eneo la miji kama Moshi, arusha na vitongoji vyake. Ukiwa umepambwa kwa theluthi iliyokuwa ikimeremeta kileleni, Kilimanjaro ulisimama pale, peke yake, kama mfalme aliyevalia taji lake ambaye hakuwa na mpinzani. Hapana, alionekana zaidi kama malkia mwenye majivuno, aliyevalia mapambo yake yote, ambaye hakupenda kujichanganya na watu wengine. Sijui ningeukodolea macho kwa muda gani mlima huo kama nisingehisi kushikwa bega huku sauti ya mtu mmoja ikisema, “Angalia, yasije yakakukuta yaliyomkuta Rebmen kwa kuushangaa mlima huo.”

Nikazinduka. Nikayaondoa macho yangu toka kileleni na kumtazama msemaji. Alikuwa mpita njia tu, mvulana aliyevaa mavazi ya shule, mfuko wa madaftari yake ukiwa kwapani. Alikuwa akitabasamu.

“Rebmen gani?” nilimuuliza.

“John Rebmen. Yule Mjerumani aliyekuwa Mzungu wa kwanza kuutia machoni mlima huu,” alifafanua.

Nikalikumbuka jina hilo. Nikakumbuka pia tarehe na mwaka ambao Rebmen aliuona mlima huo kwa mara ya kwanza. Ilikuwa Mei 11, 1848.

“Rebmen alifanya nini?” niliuliza.

“Hukumbuki?” mwanafunzi huyo alinihoji. “Hukumbuki yaliyompata? Hukumbuki kuwa aliibiwa mfuko wake uliokuwa na fedha zake, nyaraka zake na kumbukumbu zote za safari yake? Ulivyokuwa umeduwaa pale wewe pia ungeweza kuporwa huo mfuko wako bila kujijua”

Nikacheka. Nilikumbuka kusoma tukio hilo kwenye kitabu cha mwandishi mmoja. Nadhani alikuwa Rebmen



mwenyewe aliyeandika. Kwamba akiwa Kilimanjaro, maeneo ya kibosh, aliibiwa mfuko wake uliokuwa na fedha zake zote na nyaraka zake zote muhimu. Siku hizi watani wa Wachaga, hasa Wapare, hulitumia tukio hilo kuwadhihaki Wachaga kuwa kwa ajili ya tukio lile Rebmen aliyekuwa mmisionari aliwalaani hata wakawa watu wa kupenda na kuabudu sana pesa kuliko utu. ‘Mchaga mzuri ni aliyekufa tu,’ ni moja ya kauli zinazoendana na utani huo.

Ingawa sikumbuki kama kweli Rebmen aliibiwa wakati akiushangaa mlima lakini bado nisingeweza kumlaumu. Kwa mtu kama yeye, aliyetoka mbali sana na ambaye hakupata kusikia wala kuona picha ya mlima huo kama mimi, kuduwaa kiasi cha kuibiwa begi lake kamwe lisingekuwa jambo la ajabu. Kitendo cha ardhi kuchomoza hadi meta 5894 juu usawa wa bahari, huku ukiwa umesimama peke yako siyo jambo la kawaida. Aidha, ile theluji kileleni na historia ya milipuko ya volkano katika vilele vyake vitatu vya Kibo, Mawenzi na Shira ni sababu nyingine za kihistoria ambazo zitamfanya mtazamaji aukodolee macho hata kuweza kuporwa begi lake.

Hata hivyo, kauli ya mtoto yule wa shule ilinifanya nianze tena kutembea mitaani, begi mkononi, macho yakiwa hayakomi kurudi kwenye kilele cha mlima mara kwa mara.

Mji huu wa Moshi, ulio mbali kwa kilomita 580 toka Dar es Salaam na 76 toka Arusha, uko kilomita 890 toka usawa wa bahari. Hesabu ya watu wa mwaka 1948 ilionyesha kuwa mkoa mzima wa Kilimanjaro ulikuwa na idadi ya watu wapatao 267,700.

Hiyo ilikuwa sehemu ya akiba yangu ya kumbukumbu juu ya Kilimanjaro. Sehemu nyingine ilikuwa juu mkazi mkuu wa mkoa huo, Mchaga. Wakati watu wengi walifahamu




kuwa Wachaga ni kabila moja, linaloongea lugha moja, mimi nilikuwa na taarifa tofauti. Wakiishi kusini mwa mlima Kilimanjaro Wachaga ni mkusanyiko wa makabila mbalimbali, wanaozungumza lugha mbalimbali wakiwa wametoka katika maeneo mbalimbali kwa nyakati mbalimbali. Watu hawa, ambao kwa bahati wote ni wabantu, baadhi yao wanafananishwa na Wakamba wa Kenya kwa siha na lafudhi. Wengine wanafaninishwa na wataveta na hata watu wa Niger na Kongo. Wataalamu wanahisi watu hawa walivutwa na hali ya hewa, mbali na utajiri wa misitu kwenye mteremko wa mlima tangu karne ya kumi na saba. Hali iliyowawezesha kuwa wakulima wakubwa wa mibuni kama zao la biashara na migomba kwa ajili ya chakula.

Miongoni mwa makabila yanayounda Wachaga ni pamoja na Warombo, Wamachame, Wavunjo na Wamarangu. Inaaminika kuwa katika zama zile za kuhamia Kilimanjaro makabila haya, ambayo yalikuwa na falme tofauti kama zilivyo lugha na tamaduni zao walipigana vita mara kwa mara. Kabila jingine maarufu Kilimanjaro, Wapare, lilitumia fursa hiyo kwa manufaa yao kiuchumi. Inaaminika Wapare walikuwa wafua vyuma mashuhuri ambao koo mbalimbali za Wachaga ziliwategemea kuundiwa silaha mbalimbali kama mikuki mishale na mapanga kwa minajili ya kujipatia ushindi dhidi ya koo nyingine.

Nilijikumbusha hayo wakati nikitembea taratibu toka kituoni hapo nikifuata barabara ambayo sikuifahamu, wala sikuwa na haraka ya kuifahamu. Nilikuwa nimejikumbusha nguo zangu za kazi, kaptula na shati la kaki murua ya Marekani, viatu vizito vya dhoruba na soksi nyeusi. Nywele zangu, kama kawaida, zilikuwa fupi zilizochongwa vizuri. Nadhani




nilionekana mrefu kuliko watu wengi eneo hilo. Nadhani pia ngozi yangu ya maji ya kunde, usafi wa mwili wangu na utulivu wangu wakati nikivuta hatua moja baada ya nyingine kutoka kituoni hapo ni miongoni mwa vitu vilivyovutia macho ya wapita njia dhidi yangu. Niliona nikitazamwatazamwa kuliko kawaida, baadhi ya watu walinong’onezana huku vidole vikielekezwa kwangu.

Halafu likatokea jambo ambalo halikupata kutembelea fikra zangu. Kundi kubwa la kinamama liliibuka toka mahala fulani kituoni hapo na kunifuata mbio. Waliponifikia walianza kuimba huku wakipiga makofi na vigelegele.

Babaaa baba huyoo…. Babaa baba huyo…. Baba…

Sikuelewa. Nilisimama na kugeuka huku na huko nikitazama nani anapokelewa na kushangiliwa kiasi hicho.

Hakuwa mwingine zaidi yangu. Walikuwa tayari wamenizingira, mfuko wangu ukapokonywa na mama mmoja kuamua kuubebea yeye. Waliendelea kuimba.

“Karibu sana baba,” mmoja wao alisema huku akinikumbatia.

Nilizidi kuchanganyikiwa. Ama wana wazimu ama mimi napata wazimu! Niliwaza nikijaribu kujibabadua toka katika mikono ya mama huyo.

“Vipi… kuna nini?” nilijaribu kuuliza. Sikusikika. Kelele zilikuwa nyingi. Yule aliyenikumbatia kwanza aliwageukia wenzake na kuwaambia, “Mnaona? Niliwaambia ni mtu mwenye haya sana.” Akawageukia vijana wa kiume waliokuwa kando na kuwauliza, “Mbona hamchangamki? Mpokeeni kishujaa shujaa wetu.”

Kauli hiyo ilifuatiwa na vijana hao wa kiume kunivamia,



wawili kati yao wakaniinua na kunibeba juu wakiniongoza njia kunipeleka walikokujua. Katika maongezi yao nilisikia mmoja akisemea, “Nilidhani Nyerere ni jitu kubwa, linalotisha na kuwatetemesha wakoloni. Kumbe ni mtu wa kawaida…”

Ndipo nikaeleka. Walikuwa wamenifananisha na Nyerere!

Wakati huo vuguvugu la kudai uhuru likiwa linazidi kupamba moto majina ya akina Julius Nyerere, Oscara Kambona, Bibi Titi Mohamed na wengineo yalikuwa yametawala sana katika vyombo vya habari. Nyerere, ambaye wakati huo alikuwa mwalimu wa shule moja ya sekondari kule Tabora alifahamika zaidi kutokana na maandishi yake katika vyombo vya habari hasa magazeti akiwa msomi aliyefika hadi Makerere, Uganda. Nyerere aliwaandaa Watanganyika kujitawala. Alisema na alisikika sana.

Sikupata kufikiria kama ingetokea siku mimi, Kiguu na Njia nikapokelewa kwa heshima kiasi hicho. Hivyo, lazima nikiri kuwa kwa kiasi fulani nilifurahia nafasi hiyo ya kubebwa. Lakini pia, kwa ajili ya kelele na imani yao kuwa nina haya nilijua wasingeamini chochote ambacho ningewaambia. Nikaamua kutulia tuli juu ya mabega yao nikicheka kimoyomoyo.

Msafara huo uliishia katika nyumba moja ya wageni, mtaa wa tatu kutoka katika kituo hicho. Nilipelekwa moja kwa moja katika chumba maalum kilichoandaliwa kwa ajili ‘yangu’. Kilikuwa na bafu na choo chumbani humo. Mfuko wangu wa safari tayari uliwekwa juu ya meza, salama salimini. Yule mama aliyejipa uenyeji zaidi yangu alisema, “Baba, oga upumzike kidogo. Bibi Titi alifika jana. Nitamwarifu juu ya ujio wako, pengine mtapenda kuteta kidogo kabla ya kuanza safari ya Machame. Chifu Abdieli Shangai atakuwa tayari




amewasubiri.”

“Lakini mimi sio Nyerere,” nilimwonya. “Naitwa…” hakusubiri hata nitaje jina langu. Badala yake aliangua kicheko, akipuuza alichokichukulia kama mzaha wangu. Akatoka huku akiufunga mlango nyuma yake.

Sikuwa na jinsi. Nikaoga. Nikapaka mafuta na kuvuta zile nguo zangu za safari. Nikavaa suruali na shati safi. Nikatia tai na koti juu. Nilifanya hayo kwa uangalifu mkubwa bila kuchafua bafu wala kuvuruga kitanda ili mweye chumba chake halisi atakapotokea akikute kikiwa kisafi.

Wakati nikijiandaa kutoka, nikiwa na dhati ya kuwahakikishia kuwa mimi sikuwa Nyerere, mlango uligongwa nikaufungua. Bibi Titi Mohamed alikuwa pale. Sikuhitaji kutambulishwa. Alikuwa mwanamke mfupi, mnene, mwenye macho maangavu.

“Julius, umeruka kwa ndege? Nilidhani ungefika hapa jioni,” alisema kwa sauti yenye mamlaka. Sauti hiyo ilififia ghafla aliponitazama usoni na kubaini kuwa mimi sikuwa Julius Nyerere waliyekuwa wakimtegemea.

“Nimejitahidi sana kuwaambia mimi sio Nyerere, hawakukubali,” nilijitetea. “Ni kama nimetekwa nyara na kuletwa hapa,” niliongeza.

Bibi Titi aliangua kicheko. Aligeuka kuwatazama wenyeji wetu waliosimama nyuma yake kunisubiri. Kicheko chake kilizungumza kila kitu. Akageuka tena kunitazama, “Pole sana bwana. Ni kweli umefanana sana na mwalimu. Kwa mtu asiyemfahamu vizuri kuwafananisha si ajabu.”

Sikumjibu. Sikuwa na la kujibu zaidi ya kutabasamu.

“Ulikuwa ufikie wapi?” aliniuliza.

“Nilikuwa natafuta mahali pa kupanga.”




“Basi unaweza kulala hapa,” aliniambia. “Malaika wako amekwishakukuongoza hadi chumbani humu, huna sababu ya kupingana naye. Pumzika, baadaye tutakaa tuzungumze. Si ajabu mola kakuleta mikononi mwetu kwa sababu maalum.”

Sikuwa na sababu ya kukataa.


* * *?

Kwa mujibu wa maelezo niliyoyapata baadaye, vuguvugu la wagombea uhuru nchini, chama cha TANU ambacho kilikuwa kimeanzishwa kutokana na TAA kulikuwa na matatizo katika kanda hiyo ya mashariki, hasa Kilimanjaro. Kwa mujibu wa maelezo hayo, matatizo hayo hayakuhusiana na chama kukubalika au kutokukubalika eneo hilo bali yalitokana na mvutano ndani ya Wachaga wenyewe.

Baada ya ule mvutano na mapigano ya makabila mbalimbali yanayounda Uchaga ulifika wakati pamoja na kukubaliana kuwa kitu kimoja. Uamuzi huo ulifuatiliwa na kumteua Mangi mkuu kama msimamizi na msemaji rasmi wa masuala ya Wachaga. Mangi mkuu huyu aliyekuwa na makao yake huko Marangu aliwekwa juu ya viongozi wengine wote wa kikabila.

Hata hivyo, ule mzimu wa chuki na kutokutamaniana miongoni mwao, ingawa ulizikwa, bado haukufa. Ni kama ulizikwa hai. Ujio wa Mjerumani, ambaye alifuata nyayo za mpelelezi wao Rebmen, ulifanyika Kilimanjaro iwe chaguo lao la awali, wakati machifu wengine wakisita kuwapokea. Mangi Sina wa Kibisho, miaka ya 1890 akiwa amejizatiti kiuchumi kwa kilimo na ufugaji, alikuwa pia ameimarisha jeshi lake ambalo lilikuwa kero kubwa kwa utawala wa wajerumani. Awali ya hapo Wajerumani hao, chini ya uongozi wa Karl



Peters, waliendesha utawala wa kinyama na ukatili mkubwa Kilimanjaro, hali iliyopelekea April 25, 1897 gavana huyo katili afukuzwe kazi na serikali yake.

Lakini miaka mitatu baadaye, Machi 2, 1890 Wajerumani hao waliwanyonga hadharani, mjini Moshi, viongozi tisa wa kikabila. Viongozi mashuhuri kati ya waliopoteza maisha siku hiyo wakiwa Mollelia wa Kibosho, Ngalami na Meli wa Moshi. Madai ya Wajerumani kwa kitendo hicho yakiwa kwamba viongozi hao walikuwa wakiwavurugia jitihada za uongozi wao Kilimanjaro.

Hivyo, mkataba ambao Mangi Rindi wa Chaga aliingia na Mjerumani miaka mitano kabla ya kitendo hicho cha kikatili, na kuufanya mji wa Moshi kuwa kituo kikubwa cha biashara ya ndovu na watumwa kati yake na Zanzibar, lilikuwa pigo jingine katika jitihada za kuifanya Kilimanjaro kuwa na sauti moja.

Ujio wa vuguvugu la kupigania uhuru kukawa kama msumari wa mwisho kwenye jeneza la jitihada hizo. Wakati huo tayari yakiwepo malumbano makubwa ya iwapo kulikuwa na uhalali na haja ya Mangi mkuu kuendelea kutoka katika ukoo na kabila moja na cheo hicho kiende kwa kupokezana au la. Mangi mkuu, wakati huo Chifu, Thomas Mareale na kambi yake walishikilia msimamo wao. Kwa upande mwingine, machifu kama Abdiel Shangali walilipinga hilo kwa vitendo. Wasomi wengi wakiwa nyuma yake, Shangali alitumia fursa hiyo ya mparanganyiko kuunga mkono TANU na kuwekeza kimsimamo mikononi mwa mkewe Solomon Eliofoo, aliyekuwa ametokea masomoni Uingereza na Marekani na kurudi na kuazishwa tawi la TANU Machame.




Lilikuwa tatizo zito kwa Chifu Mareale. Jitihada zake za kuwekeza kwa Petro Njau hazikuzaa matunda yaliyotarajiwa, hali iliyopelekea uhusiano wake na TANU ulegelege. Ingawa yeye binafsi aliwasiliana sana na Nyerere na wakati fulani kumtaka aje Kilimanjaro kuzungumza na Machifu wote bado alionekana kama mtu aliyekuwa njia panda. Hali ambayo baadaye ilishusha umaarufu wake, lakini hadhi yake na nafasi yake katika historia kamwe haikupata kufutika.

Kwa upande mwingine, Kilimanjaro haikuwa na njaa sana ya uhuru kama zilivyokuwa sehemu nyingine za Tanganyika. Kiuchumi alikuwa mbali zaidi. Kilimo cha mibuni kilikuwa kimeanzishwa katika eneo hilo tangu mwaka 1919 na kushika kasi 1930 na kuendelea. Hali hiyo iliambatana na kuanzishwa kwa vyama vya ushirika, ikiwa nchi ya Kwanza Afrika kuwa na mfumo huo. Hali ya hewa na ujio wa mapema wa wakoloni katika maeneo hayo pia ilikuwa neema nyingine kwao. Walipata shule nyingi na bora zaidi mapema.

Huduma za matibabu, barabara na maji pia walizijua

kabla ya maeneo mengi ya nchi kufikiriwa.

Hivyo, inaweza kueleweka pale ‘Mshumbue’ Mangi mkuu Thomas Lenana Mlanga Mareale II aliponukuliwa akishuku kuwa Nyerere ‘alikuwa akinikwepa,’ na kwamba alimsahau katika harakati za uhuru. Hata hivyo, Mangi mkuu huyu aliendesha harakati mbalimbali za kisiasa ndani na nje, ikiwa pamoja na kumlipa wakili ambaye alimtetea Kenyatta wa Kenya hadi akaachiwa toka kifungoni wakati akituhumiwa kujihusisha na Mau Mau.

“Hivyo, ni sehemu fupi ya historia ya uchagani kaka yangu,” Bibi Titi Mohamed alisema baada ya maelezo hayo ambayo niliyaunganisha na kujaribu kuyaweka katika mtiririko






mmoja baada ya huyu kusema hili, huyu lile nikijumuisha na yale yaliyokuwa katika kumbukumbu zangu.


Tulikuwa katika ukumbi wa hoteli hiyo. Watu wapatao wanane, wakiwemo wanawake watano, Bibi Titi na wawili wengine kati ya wale walionipokea pale kituo cha mabasi. Nilionekana kama muujiza. Nadhani hata kama angekuwa Nyerere mwenyewe hangepata idadi kubwa ya watu waliokuwa wakiingia na kutoka kwa nia ya kumwona ‘mtu aliyefanana na Nyerere’. Wingi wa watu hao wakiwa kina mama ambao walicheka na kujicheka sana kwa kosa la kunichanganya na kijana huyo aliyekuwa akitajwatajwa sana. Nadhani kwa namna fulani walidhibitiwa, kwani baadaye tuliketi na kuingia katika maongezi marefu, yaliyoongozwa zaidi na Bibi Titi, mwanamama msemaji sana, mwingi wa vichekesho huku akiwa pia msikilizaji mzuri.


“Wachaga wana historia tofauti na sehemu nyingi za nchi,” Bibi Titi aliongeza. “Sisi watu wa Pwani tuna historia inayotofautiana kwa kiasi kikubwa na wao. Nadhani wageni wengi waliotembelea makwetu toka enzi za enzi waliacha athari nyingi miongoni mwetu zaidi ya Uchagani ambako ni mbali kutokea Pwani.”


“Nadhani,” niliunga mkono. “Maana toka Waarabu, Wareno, Wajerumani na baadaye Waingereza wenyeji wao wa awali ni nyie tu.”


“Bibi Titi alitabasamu. “Tuyaache hayo,” alisema. “Hebu na wewe tuambie yako tukusikie. Ilikuwaje ukafananishwa na bwana Julius?” alinihoji.


“Kwa kweli sijui. Simjui Julius wala sijapata kumtia machoni labda imetokea tu tukafanana maana duniani wawili wawili,” nilimjibu.





“Huna udugu naye?” “Hata kidogo.” “Wewe ni Mzanaki?” “Wala.”

“Kumbe nini basi.”

“Mie Muha. Natokea kigoma.”

Hufanani na Waha. Utakuwa Mmanyema.” Bibi Titi alidai. “Lakini hilo halina haja kwa sasa,” aliongeza. “Kama hutajali, tuambie wewe ni nani, unatokea wapi na unaelekea wapi.”

Nikawatajia jina langu. Nilitaja pia kazi niliyowahi kufanya ambayo sasa sikuwa nayo. Walivutiwa na taarifa ya safari za hapa na pale katika miji na vijiji mbalimbali vya Bonde la Ufa pamoja na mbuga za wanyama.

“Hujapata kufikiria kujiunga na harakati za kupigania uhuru?” Bibi Titi aliuliza. Akaongeza, “Maana wewe unaonekana ni mtu wa watu. Halafu, unatembea sana. Lakini la muhimu zaidi ni kwamba tungependa kupata mtu wa kwenda kuhamasisha harakati hizi huko kwenu. Ndiyo kuna watu tayari, lakini hawatoshi. Kumg’oa mkoloni siyo mchezo. Inahitajika kila silaha na kila askari.”

Wazo hilo halikupata kunitembelea akilini. Sikuwa na hakika kama mimi ni mtu wa kupanda jukwaani, mbele ya kadamnasi na kuanza kujinadi kuwa mimi ni bora zaidi ya wengine, au kumnadi mtu mwingine kwamba anafaa kuliko mwingine. Kwa ujumla sikupata kuwa na ndoto ya kuwa mwanasiasa maishani mwangu.

Bibi Titi alisoma hayo katika macho yangu. Akatabasamu. “Ni jambo linalohitaji kulifikiria.” Alinena. “Harakati zetu bado ni changa. Hakuna fedha za kulipa mtu wala kulipwa. Kwa




ujumla tunajitolea. Tunachopigania ni uhuru. Ukipatikana kila mtu atakula matunda ya uhuru.”

Alisita, akaitazama saa yake. “Nadhani basi alilopanda Mwalimu linakaribia kufika. Nisingependa akina mama wakampokee mtu mwingine wa watu na watu. Naenda mwenyewe kumpokea. Atafikia hoteli hiihii. Nitakukutanisha naye, pamoja na Kambona, ili uzungumze nao. Nadhani utakuwa tayari umefanya uamuzi.”

Akainuka na kuondoka, alifuatana na wale kina mama wengine na wanaume wawili.

Nilibakia na watu wawili mmoja alikuwa mtu mfupi, mweupe, ambaye kama si kwa ajili ya mvi mbili tatu kichwani ungeweza kumfikiria kuwa ni mtoto mdogo, ingawa umri wake ulizidi wangu kwa mbali sana. Hakuonekana kuwa Mchaga. Na hakuchelewa kunithibitishia hilo pale alipozungumza na mara moja nikabaini lafudhi yake kuwa ya Kipare zaidi.

“Nikweli miminiMpare,”alijibu swalilangu.“Nimeungana hawa watani wangu wajanjawajanja, katika harakati hizi za kupigania uhuru. Tatizo ni hapo utakapopatikana huo uhuru. Mchaga atapenda kuuteka nyara uwe wake, maana Mchanga mzuri ni yule aliyekufa tu.” Alisema akimtazama Mchaga.

Yule Mchaga akacheka. Yeye pia alinizidi umri. Alikuwa amevaa suti ya kijivu, tai shingoni na alishikilia mkoba wa nyaraka mkononi. Uso wake uliojaza ulipambwa na miwani. Hali iliyompa sura ya usomi.

“Achana na wajukuu wetu hao,” aliniambia. “Hao wameshindikana kabisa. Mpare anapata kesi ya kuku, ama kwa kuiba au kuibiwa. Atauza hata ng’ombe ili ashinde kesi hiyo. Kuna mtu hapo?”

Mie pia nililazimika kucheka.



soda.


Waliagiza vinywaji. Wao walikunywa bia mimi nilikunywa


“Bia?” alihoji mmojawao. “Sinywi.”

“Kwa nini? Unaumwa?”

“Hapana. Sijawahi kunywa toka nizaliwe.” Walinitazama kwa mshangao kana kwamba


nimewaambia jambo la ajabu kuliko yote waliyopata kuyasikia. “Kwa umri huo?” Yule Mchaga aliuliza, “Huo ni umri wa


kunywa vitu vya kiutu uzima.” Aliongeza.


“Tatizo ni kwamba sijapata kuitamani wala kuifiria.


Halafu bei yake kubwa mara tatu kuliko soda.” Nilijitetea. “Acha ubahili wa Kipare,” Mchaga alisema akicheka.


Mpare alicheka pia. Lakini alihamisha maongezi na kunitaka nimsimulie juu ya safari zangu za maporini. “Huko ulikokwenda kuna wanyama?”


“Wengi tu.” Nilimjibu “Unaweza kukutana na kundi la nyati wengi kama Ng’ombe wanaofugwa, kundi la twiga utadhani wako kwenye maonyesho na pundamilia kana kwamba wana sherehe.”


“Tembo?”


“Wengi kupita kiasi” “Vifaru?”


“Wengi tu.”


“Umepata kuwaona kwa macho yako?” “Mara nyingi tu.” Nilimjibu.


Mchaga alijaribu kuingilia kati, lakini Mpare alimkatisha kwa maswali yake juu ya wanyama na maeneo tuliyotembelea. Nilipomtajia kuyafahamu kwangu vyema maeneo ya Manyara, Ngorongoro na Tarangire alionekana kuvutiwa zaidi. Nilihisi



kuona dalili za udenda zikielekea kudondoka toka mdomoni mwake. Sikuwa na hakika kama niliona vizuri.

“Itabidi tuzungumze kama wanaume baadaye,” aliniambia. “Unatarajia kuondoka lini?”

“Sina haraka,” nilimjibu. “Nitapenda kufika Arusha pia

kabla ya kurejea maporini,” niliongeza.

“Nitakupeleka.” Alidakia. “Mimi ni mwenyeji Arusha kuliko hapa Moshi. Hutohitaji kulala au kula hotelini.”

Mchaga aliangua kicheko cha dhihaka, kicheko kilichofuatiwa na “Ndugu yangu umekwisha. Mpare ajitolee kukupeleka Arusha, akupe malazi na chakula! Kuna jambo hapo,” alisema.

“Atakwisha yeye,” nilijibu, “Maana siye Wamanyema tuna historia ya kula watu. Nitamla mzimamzima kabla yeye hajanila,” kauli ambayo iliniangusha kicheko kirefu.

“Lakini Wapare unawajua vizuri? Wana maradhi yasiyo na dawa ya uchoyo. Wewe na yeye mtakufa njaa hata kabla hujafikiria kumla, huku mkiwa na fedha mfukoni,” aliongeza na hivyo kuongeza kicheko. Sikujua mengi juu ya Wapare zaidi ya ukweli kuwa ni kabila jingine kubwa la Kilimanjaro, wanaishi katika miteremko ya milima ambayo ni sehemu ya mlima Kilimanjaro, na kwamba wao pia wamegawanyika katika sehemu kuu mbili, Wapare wanaozungumza Kingweno, wanaoishi kaskazini na Wachasu waishio Usangi, Kusini. Lugha zao zina aina fulani ya kulandana na zile za Wataveta na Asu wa Kenya.

Enzi za kale Wapare walisifika kwa uganga wa mvua na uhunzi. Uhakika kuwa kabila hili ni la kale ni pale nilipowahi kuona kitabu kitakatifu cha Biblia iliyoandikwa kwa lugha ya Kipare, kilichochapishwa mwaka 1910. Pamoja na ujio huo




wa dini za kisasa Wapare waliendelea na tiba mbalimbali za asili kama maziwa ya Konda badala ya mama kumtibu mtoto mwenye wintu, maradhi ya sangasi yaliyoharibu vinywa vya watoto, majani yaliyoitwa more yaliyotibu ‘Kirumu,’ ‘kiruti’ au ‘kinyoka’, maradhi ya macho kwa watoto wadogo.

Historia ya dini za kigeni Upareni inaanza na mmisheni Jakob Janssen Dannholz, Mjerumani wa madhehebu ya kiluteri ambaye mwaka 1908 alianzisha ‘kazi ya bwana’ huko Mbaga, Upare ya kusini. Aliishi hapo hadi mwaka 1907 alipokamatwa na kuchukuliwa na Waingereza kama mfungwa wa kivita hadi katika kambi yao ya Misri ambako alifariki mwaka mmoja baadaye. Alifariki na umri wa miaka arobaini lakini kazi aliyoianzisha iliishi, ikakua na inaendelea kukua hadi leo.

Kinyume na makabila mengi nchini, wanawake wa Kipare walikuwa mstari wa mbele, pengine kuliko wanaume zao, katika harakati za kupigania uhuru na haki zao. Kumbukumbu zangu toka vitabuni zilinikumbusha mwaka 1946, kule Usangi, pale maelfu ya akina mama walipoibuka na kuanzisha vurumai kubwa wakipinga kulipa kodi. Tukio hilo liliibuka pale Chifu mmoja alipotembelewa na mkuu wa wilaya kwa ajili ya majadiliano. Umati wa wanawake wapatao mia tano waliizingira nyumba hiyo kutaka ufafanuzi juu ya utaratibu wa kodi ambao hawakuafikiana nao. Mkuu huyo alipojaribu kuondoka bila kuwapa ufafanuzi walipandwa na hasira, walianzisha nyimbo huku wengine wakiipiga mawe nyumba hiyo ya Chifu. Tukio hilo lilifuatiwa na maelfu ya wanawake kujiunga katika vuguvugu hilo ambalo lilitikisa serikali ya mkoloni.

Kama Wachaga, Wapare pia walikuwa katika mstari wa






mbele katika kuiunga mkono TAA na baadaye TANU katika mapambano ya kudai kujitawala. Hali hiyo inachukuliwa kuwa ilisaidia kuondoka wazo la kuibuka kwa chama cha kikabila ambacho kingeweza kuwa chini ya ‘PARE UNISI’ ambayo ilikuwa na nguvu nyingi kutokana na mchango wa kiuchumi iliyotokana na kilimo cha mibuni, katani na chai.


“Unasemaje?”


Mpare alinizindua. Nikamtazama.


“Naona uko mbali sana,” aliongeza. “Nilikuuliza unadhani tuondoke lini kwenda Arusha?”


“Nilikuambia sina haraka, kwani hatuonani tena baada ya leo?” nikamuuliza.


“Tutaonana. Bila shaka yoyote.”


Mara akina mama walikwenda stendi kumpokea mwalimu wakaanza kurudi, mmoja baada ya mwingine. Hawakuwa na furaha kama ile waliyoonyesha wakati wakinipokea mimi. Hatukuchelewa kuelewa sababu.


Mwalimu Nyerere hakutokea.


Mchaga aliyekuwa kimya muda mwingi, akishughulikia kinywaji chake alitabasamu kidogo akinitazama. Kisha akasema, “Maadam Nyerere hakuja, na wewe umefanana naye, tutaendelea kukuita Nyerere. Unasemaje?”


Sikumbuki kama nilimjibu.



SURA YA KUMI NANE?

Za Moshi?


oshi na Arusha ni miji jirani sana, ikiwa imetenganishwa kwa umbali wa kilometa 75 tu na hivyo kufanya safari toka mji huu hadi

ule iwe takriban dakika sitini kwa gari lisilo na matatizo.

Safari ya Arusha na Moshi ni burudani tupu. Japo barabara haikuwa nzuri sana, lakini kule kupita katikati ya mashamba makubwa ya mibuni na migomba, vijiji vichache vikichomoza hapa na pale ilikuwa burudani ya macho. Ilikuwa alfajiri moja tulivu na angavu sana. Anga lilitakata pasi ya wingu lolote. Jua lililokuwa likichomoza Mashariki liliufanya mlima Kilimanjaro ambao tuliupa kisogo usimame pale, taji lake jeupe kichwani, juu ya kiwiliwili chake cha kijani, ukiwa umetuinamia kama mzimu au malaika aliyekuwa akitutakia heri katika safari yetu. Sikuchoka kugeuka mara kwa mara kuutazama uzuri huo wa pekee.

Hata kabla Kilimanjaro haujatokomea nyuma yetu, ulijitokeza mlima mwingine mbele yetu. Kama Kilimanjaro, ulisimama kando ya mji wa Arusha, kwa maringo na utukufu wa aina yake. Japo mbele ya Kilimanjaro mlima huu ulikuwa kama mtu na mdogo wake, bado utukufu wake ulikuwa palepale. Sikuhitaji kuambiwa kuwa huu ulikuwa mlima




Meru, fahari nyingine ya Tanzania. Ukiwa umepanda juu ya usawa wa bahari kwa mita 4565 mlima huu ulimwaga hewa safi yenye ubaridi mwanana uliopenya katika miili ya wakazi wa Arusha na vitongoji vyake hadi kuitikisa mifupa ya wageni wa mandhari hiyo.

“Naona tayari umeanza kumsahau mrembo mmoja umeanza kumtamani mrembo mwingine. Vipi, unafikiria kumpanda?”

Nikazinduka na kumtazama msemaji. Alikuwa rafiki yangu mpya, yule Mpare, ambaye toka tukio lile la mimi kufananishwa na Nyerere na kumsimulia kwa ufupi maisha yangu ya maporini aliniganda kama kupe. Siku zote tatu nilizokaa mjini Moshi alikuwa nami kama kuku na vifaranga vyake. Sikupata kujiuliza nani alikuwa kuku nani kifaranga kati yetu. Lakini ile tabia yake ya kuwa nami bega kwa bega, tukiachana wakati wa kulala, nikiamka tayari ananisubiri, nilianza kupata hisia pamoja na yeye kujifanya kuku ilielekea kuwa yeye ni kifaranga asiyetaka kumpoteza mama yake.

“Mrembo gani?.... Kumpanda nani?” nilimuuliza kwa mshangao.

“Mrembo Kilimanjaro, dada mtu. Mara tu ulipomwona mdogo wake, Meru, tayari umehamishia mapenzi yako kwake. Hilo liko wazi katika macho yako. Ukipenda tunaweza kufanya mipango tuupande. Sio mrefu kama Kilimanjaro,” alijibu.

Niliyatafakari maneno yake kwa muda. “Kama ningepata fursa hiyo ningeitumia kupanda mama wa milima yote Afrika, mwenye sifa zote za pekee duniani, Kilimanjaro; ili nipate kitu cha kuwasimulia wajukuu zangu pale nitakapozeeka,” nilimweleza.

“Wajukuu! Uliniambia hujaoa.”






“Iko siku nitaoa. Nitapata watoto na baadaye wajukuu,” nilimjibu, jibu ambalo lilifanya mada hiyo iishie hapo.




* * *?


Arusha ilinisisimua kwa mengi. Mji mdogo ndiyo, lakini ulikuwa na pilikapilika nyingi, wageni wengi. Ukiwa mji wa mpakani, ukiwa umetenganishwa na Nairobi kwa kijiji mashuhuri cha Namanga. Wageni wengi walioitembelea Arusha walikuwa wafanyabiashara, watalii na wataalamu mbalimbali wakiwa katika pilikapilika hii na ile. Wahindi wachache walikuwa na biashara zao lakini sehemu kubwa ya biashara ilishikwa na wenyeji, Wachaga, Wapare na Waarusha wachache.


Wamasai walinisisimua pia. Ingawa kiasili wao ndio wenyeji hasa wa mji huu lakini kama wanavyoishi mbungani ndivyo walivyokuwa wakiishi hapa. Siku zote walionekana wageni wa mji, wakifanya kazi yao nje kabisa ya mji ambako wao na ng’ombe wao walijiona huru zaidi. Hata ujio wao mjini kwa mahitaji muhimu kama chumvi na vipande vya nguo walivyozowea kuvaa, bado vaa yao, upande mmoja wa mwili ukiwa wazi, sime kiunoni kana kwamba muda wote wako vitani huku kiswalhili na lugha nyingine zinazotumiwa na wengi kikiwapiga chenga. Kuwepo kwao mjini kulifanya waonekane kama watu waliopotea njia.


Mpare, wakati fulani aliponiona ninavyowashangaa, alinisimulia kisa kimoja cha kuchekesha juu ya Wamasai. Kwamba katika jitihada za kuwalazimisha kuvaa nguo za kisasa serikali ilipata kutoa amri ya wauzaji wote wa maduka kutomuuzia kitu Mmasai ambaye hakuvaa ama suruali ama kaptula ndani ya shuka lake.





Hatua hiyo iliwaudhi sana Wamasai. Hata hivyo, ili wapate huduma hizo kijiji kilibuni mbinu ya kununua kaptula moja ambayo kila aliyekuwa na shida mjini aliiazima. Kwa aibu, kaptula hiyo ilivaliwa nje kabisa ya kijiji. Na baada ya manunuzi anaporejea nyumbani Mmasai aliivua kaptula hiyo nje ya kijiji kabla ya kuirejesha.

Sikushangazwa kabisa na habari hiyo, kwa jinsi nilivyowafahamu Wamasai.

Kama ilivyokuwa Moshi, Mpare hakuwa Mpare wa kawaida Arusha vilevile. Hatukulala hotelini. Alinipeleka kwa ndugu zake, maeneo ya Kaloleni ambako alinitambulisha kama rafiki yake ‘mpenzi.’

Alinitembeza maeneo mbalimbali ya mji, Oljoro, Kijenge, Mianzini na kwingineko. Alinifikisha hadi Namanga, Mpakani, ambako alijaribu kuomba ili turuhusiwe kuvuka mpaka na kuikanyaga ardhi ya Kenya walau kwa dakika kumi, tukakataliwa. Wakati tukirejea, kwa hasira zake za kukataliwa kuvuka mpaka aliamua kubadili uelekeo wa safari yetu. “Twende zetu Ngurdoto, tuburudishe macho yetu,” alisema.

sana katika mbuga, misitu mito na ziwani. Nimeona wanyama na ndege wengi sana. Lakini sikupata kuona wanyama wa kuvutia kama tumbili weupe, lino wekundu, mbega na ndege wengi kama niliowaona Ngurdoto. Niliwaona kereng’ende, kibeti, aina mbalimbali za vibisi, kicheleko na wengine wengi ambao waliifanya Ngurdoto kuwa mahala pa kusisimua.

Mandhari ya eneo hilo pia ni kitu kingine cha kuvutia. Ikiwa karibu kabisa na mji wa Arusha, katikati ya milima mikubwa maarufu ya Kilimanjaro na Meru Ngurdoto ilikuwa zawadi nyingine ya asili kwa nchi na vizazi vyake.




Tulirejea mjini jioni sana. Kwa ushauri wake tulikula chakula cha usiku hotelini. Tukashushia kwa vinywaji. Yeye bia za moto, mie fanta mbili za baridi. Kama ilivyokuwa katika mambo mengine, alisisitiza kulipia vinywaji na chakula hicho peke yake. Nikakataa katakata na kulipia. Kisha nilimwambia, “Nadhani umefika muda wa kuzungumza ana kwa ana kama wanaume wawili. Umekuwa mwema kwangu kwa muda mrefu. Umelazimisha urafiki na udugu hadi nikaukubali. Niambie, unahitaji nini sasa kutoka kwangu?”

Mpare alitazama huko na huko kuona kama tulikuwa katika faragha. Hakuridhika. Akanishauri tuhamie katika kona ya baa hiyo iliyokuwa na meza mbili tatu zisizo na watu. Tukahama. “Nataka tuwe marafiki,” alisema baada ya kuketi.

“Nadhani tumeshakuwa.” “Nataka tuwe ndugu,” aliongeza.

“Nadhani tumeshakuwa,” nilimjibu tena.

Alisita kwa muda kabla hajasema, “Nataka tuwe wasiri. Kwa mwanamume udugu na urafiki havitoshi. Tuwe kitu kimoja. Langu liwe lako, lako liwe langu. Tuafikiane hilo kwanza, kisha tuchukue hatua ya pili.”

Nilimtazama kwa mshangao uliochanganyika na mashaka. Alikuwa akizungumza kwa makini na msisitizo kuliko ilivyokuwa kawaida yake.

“Hatua ya pili ni ipi?” Nilimuuliza.

“Nataka tutafute pesa. Nataka tuwe matajiri. Mimi nawewe,” alijibu mara moja.

“Kwani hatutafuti?” Nilimuuliza.

Swali hilo lilimfanya aangue kicheko. “Tunatafuta ndiyo. Lakini tunazotafuta ni fedha za kula tu, fedha za kubadili mboga na mashati. Mwanamume anahitaji fedha zilizotakata.




Unaona maghorofa yake yanayopanda?” aliuliza akinielekeza nje ya dirisha ambako jengo la ghorofa nne lilikuwa likijengwa. “Lile linajengwa na binadamu kama mimi na wewe.?

Nataka miaka miwili ijayo tuwe na majengo kama yale. Tuwe na magari ya maana. Tuweze hata kununua ndege.”

Nikacheka.

“Usicheke. Hii sio ndoto. Nyota yangu na yako zinafanana. Naona waziwazi mimi na wewe tukiogelea katika bahari ya pesa. Tunajenga… tunalimisha mashamba makubwa… tunakwenda kutembea Ulaya…”

Alizungumza huku akitazama angani, macho kayakodoa kama anayekiona hicho anachozungumza. Nilitamani kucheka tena, lakini kitu fuani kilinizuia. Kitu ambacho sikuweza kukipambanua kati ya hofu na mashaka juu ya rafiki yangu huyo.

“Nitakusimulia hadithi moja,” alisema ghafla. “Sio hadithi ya kupendeza sana, lakini itakufanya uelewe kwa nini nahitaji fedha za maana. Yuko bwana mmoja,” alianza hadithi yake. “Alizaliwa katika familia moja masikini sana. Kwa bahati mbaya sana, familia hiyo ilizungukwa na familia yenye kipato kikubwa, familia ambazo zilisomesha watoto wao nje ya nchi, zilijenga nyumba za maana na kushindana katika kubadili magari na mavazi. Masikini na huyu na ndugu zake wote waliishia kuajiriwa katika mashamba ya majirani hao ambao waliwanyanyasa na hata kuwapiga makofi hadharani. Hali hiyo ilimfanya jamaa huyu asononeke na kukosa raha.”

“Siku moja bwana huyu masikini alikuta baba yake akiwa amepiga magoti mbele ya mtoto wa tajiri yao mmoja, huku akisihi na kubembeleza. Kisa? Masikini baba yake alikuwa amefukuzwa kazi kwa kushindwa kufika kazini





jana yake kutokana na maumivu ya mgongo. Baba alikuwa akijaribu kumsihi mtoto huyo wa tajiri abadili uamuzi wake na kumruhusu kuendelea na kazi ya shamba. Kijana huyo hakukubali, badala yake alimtukana kwa kila neno chafu alilolifahamu hata masikini mzee akawa akitokwa na machozi.” “Ilikuwa picha ya kusikitisha sana kwa yule kijana.?

Alimfuata baba yake na kumwinua huku akimwambia, “Kufukuzwa kazi sio mwisho wa dunia. Nenda nyumbani kapumzike,” kauli ambayo yule mtoto wa tajiri aliisikia.

Akageuka na kumwambia, “Na wewe pia umefukuzwa kazi. Toka leo msikanyage katika mashamba yetu.”

“Masikini kijana yule maisha yakawa magumu sana. Alikuwa ndio kwanza ameoa na kupata watoto wawili mapacha. Alishindwa kuwalisha. Watoto wakapata utapiamlo na kufa mmoja baada ya mwingine. Mama wa watoto alishindwa kuvumilia. Alilia kwa wiki mbili. Asubuhi moja ya wiki ya tatu mama huyo alikutwa akining’inia kwenye paa la nyumba yao. Alijinyonga kwa kamba ya katani.”

“Uchungu, aibu na hasira vilimfanya baba huyo aondoke nyumbani na kwenda mjini kutafuta kazi. Hakuwa na elimu ya kutosha, hakuwa na ndugu mwenye madaraka, hivyo suala la kazi likawa ndoto. Masikini aliishia kuambulia vibarua vya hapa na pale, ambavyo havikumsaidia sana. Wakati akihangaika huko mjini alipokea habari mbaya moja baada ya nyingine. Mama yake alikuwa amefariki kwa malaria. Hakwenda, kwa aibu ya kwenda mikono mitupu. Baba yake naye akafa. Hakwenda, kwa sababu zilezile. Familia yao sasa ilibakiwa na watu watatu tu, bibi mzaa baba, kikongwe ambaye kila usiku ulipoingia waliamini kuwa kesho asingeamka kutokana na malalamiko ya maumivu ya miguu na mgongo




yaliyokuwa yakimsumbua. Wengine walikuwa wadogo zake wawili, msichana aliyekuwa kiwete na mvulana ambaye ndiye aliyekuwa akichangia kuleta walao vibaba vya unga vilivyowawezesha kuvuta siku.”

“Yule bwana, masikini, hadi leo anahangaika mijini akijaribu kushika ama hiki ama kile bila mafanikio,” alimaliza hadithi yake na kunikazia macho.

“Hii ni hadithi ya kweli,” baadaye alisema. “Na wahusika wake ni wa kweli. Mhusika mkuu ni mmi.”

“Wewe?” Niliuliza kwa mshangao.

“Naam, mimi mwenyewe. Na, kwa kweli, hicho ulichokisikia ni moja ya kumi tu ya mateso na aibu zitokanazo na umasikini ambazo nimepata kukutana nayo. Kinachoitesa roho yangu sana ni huyo bibi na wajukuu zake ambao wanaishi kwa kudra ya mwenyezi mungu. Tatizo lolote linalohusiana na pesa linaweza kumfanya yeyote kati yao au wote wapoteze maisha kama mende au kunguni mikononi mwa binadamu.”

Sikupata kujua kama nilikuwa na huruma. Lakini nilipohisi machozi yakinilengalenga kwa simulizi hiyo nilijua kuwa nimeshikwa na huruma. Akili ikahama na kunifanya niifikirie familia yangu huko Buha. Pengine ina hali kama hiyo. Pengine haipo tena, wote wamekufa kwa shida hii au ile! Chozi moja liliteleza ghafla na kulifikia shavu langu. Nililifuta mara moja kwa kiwiko cha mkono na kisha kutoa leso yangu ambayo haikutoka mkononi mwangu kwa muda mrefu.

Tulipigwa na kimya cha muda mrefu, kimya ambacho Mpare alikiondoa pale aliposema baadaye, “Ninaposema nimejaribu kila kitu maana yake ni kila kitu. Nimejaribu biashara lakini bila mtaji ni biashara gani utafanya? Nimejaribu kutafuta kazi. Bila elimu utapata kazi gani ya maana? Lilipokuja






vuguvugu la siasa na kupigania uhuru nilikuwa mstari wa mbele kujiunga, kwa matarajio kuwa nitakuwa mmoja wa wachache watakaowahi kula matunda ya uhuru. Lakini humo pia nimekata tamaa. Elimu yangu ya ngumbaru, niliyoipata kwa taabu haikufua dafu mbele ya wenzangu ambao tayari wamejipanga vizuri. Hata pale unapokuwa na wazo la maana bila elimu au pesa kamwe hutasikia wala kusikilizwa.” Alisita kwa muda. Alipozungumza tena ilikuwa kama aliyenisahau, na kuzungumza peke yake. “Nimepoteza watoto niliowapenda. Nimempoteza mke niliyempenda. Nimepoteza wazazi. Siwezi kupoteza tena nafasi ya kutajirika.”


Akanigeukia ghafla na kusema, “Nitakuwa tajiri. Nitafuta aibu zangu zote. Wewe utanisaidia. Tutapaa kama mlima Kilimanjaro. Wote waliokuwa wakitupuuza watainua nyuso zao kutushuhudia.”


“Ulisema juu ya tatizo la mtaji. Umeshaupata?” nilimuuliza.


Kwa mara ya kwanza katika kipindi kirefu nilimwona akitabasamu. “Naam, mtaji ninao tayari,” alijibu baadaye.


“Uko wapi?”


“Wewe ni mtaji.” Alijibu.


“Mimi! Nilishangaa “Unajua sijakuelewa?”


Akatabasamu tena kabla hajasema, “Utanielewa. Ni rahisi sana. Kwa ujuzi wako wa mambo ya porini, kwa uzoefu wako wa masuala ya mbugani na msimamo ambao nauona katika macho yako, naamini tukishikana ni mtaji tosha.”


Bado sikumwelewa.


Akafafanua, “Tunahitaji bunduki moja tu na risasi tano. Risasi moja ikilenga shabaha tayari tumetajirika. Bunduki ninayo, risasi ninazo. Kitu gani kitanizuia?”




Bado sikuwa nimemwelewa. Nikamtumbulia macho ya kumtaka ufafanuzi.

“Nadhani nizungumze kwa tuo. Nisikilize kwa makini, tafadhali,” alisema akijiweka vizuri juu ya kiti na kukivuta karibu yangu zaidi.


* * *?

Niliwapenda wanyama wa porini. Niliwapenda sana. Kukuru, kakara, tumbili na nyani wakicheza juu ya miti, mara waruke toka tawi hadi tawi au toka mti hadi mti, kwangu ilikuwa burudani safi sana. Niliwahusudu chui, ngozi zao za madoa yanayopendeza na mwendo wao wa maringo porini, pasi ya kishindo, kana kwamba wao ni malkia wa nyika ni mambo ambayo yalinisisimua sana. Nilivutiwa na simba, wafalme wa mwituni, kwa ubabe na jeuri yao hasa wale wa Serengeti ambao hupanda miti na kupumzika juu yake kama chui. Niliwapenda twiga na shingo zao ndefu, niliwapenda hata fisi wala mizoga. Kwa ujumla, niliwapenda wanyama wote.

Niliwapenda pia ndege, tai mvumilivu ambaye anaweza kumfuata mnyama na hata binadamu mgonjwa kwa siku kadhaa hadi atakapozidiwa na kukata roho ndipo humvamia na kumla, njiwa ambao huburudisha kwa sauti zao nzuri, korongo na jamii zake zote, korongo mfuko shingoni, korongo uso mwekundu na wengineo. Nilimpenda pia bundi na hadithi zake zenye mapokeo anuwai.

Samaki wa majini, wadudu wa ardhini pia ni viumbe niliowapenda. Kila mmoja ambaye ungemtazama kwa makini na kufuatilia nyendo zake, kama unazo fikra usingekosa kujifunza jambo toka kwao. Nyuki na malkia wao, ambao kwa umoja wao hujengwa himaya kubwa na kutuwezesha kupata




asali. Mchwa ambao pamoja na udogo wao hujenga vichunguu, kinyonga mwenye uwezo wa kubadili rangi ya mwili wake kama anavyojisikia, jongoo menye miguu elfu moja na moja lakini asiyeweza kukimbia, nyoka asiye na mguu hata mmoja, mwepesi wa kuteleza maporini kama mshale.

Zaidi ya wanyama niliyapenda mazingira yanayowawezesha kuishi: misitu murua yenye mimea na vivuli wanavyohitaji, mito na mabwawa yanayowapatia maji na hifadhi kwa wale waishio majini, mawe, milima na mabonde ambayo ni sehemu ya maisha yao na kadhalika. Licha ya mazingira haya hifadhi ya wanyama bado ni kivutio muhimu cha watalii, ambao kutembelea kwao nchini kuna maana ya kuleta pesa. Aidha, mazingira ni urithi wa watoto na wajukuu wetu ambao wana haki ya kufaidi kama tunavyofaidi sasa.

Niliwaza yote hayo nikiwa chali kitandani, usingizi ukiwa umenikimbia usiku kucha. Ilikuwa baada ya Mpare, ambaye jina lake halisi lillikuwa Daniel Mbonea.

Alikuwa ameibuka na wazo la mradi wa hatari, unaoshawishi na kutisha pamoja, mpango wa kunitaka tushirikiane katika uwindaji wa wanyama pori na kujipatia nyara ambazo zingetupatia utajiri wa harakaharaka.

“Kila kitu katika wanyama ni pesa,” alikuwa amesisitiza. “Ukimwua tembo pembe zake ni pesa. Ukimwua chui na hata mamba ngozi zao ni pesa. Lakini tunayemtaka zaidi ni kifaru. Ukiwaua wawili tu, umasikini kwa heri. Wako wengi huko mbungani. Lazima tuwatafute.”

Wazo hilo sikupata kulifikiria. Kwa kila namna lilinitisha, nikijua kuwa si kazi ya hatari kwa maisha yetu tu, bali kwa vyovyote vile ni kinyume na sheria. Nilimkumbusha hilo. Lakini Mpare alicheka tu, kisha akaniuliza, “Hivi unafahamu






hawa waliotajirika wamefanya kazi gani?” Nikamjibu kuwa sijui.


“Huwezi kujua. Hutapata kujua. Na wao hawatajua utajiri wetu umetoka wapi. Mwanamume anahitaji kuthubutu. Hii ni nafasi yetu ya pekee.”


Nilikuwa na mengi ya kufikiri. Awali ya yote lilikuwa lile pendekezo la akina Bibi Titi Mohamed la kunitaka nirudi nyumbani nikaanzishe tawi la TANU ili kujiandaa kwa uhuru ambao alisisitiza kuwa ‘umenukia.’ Kimsingi nilikuwa tayari nimeafikiana naye. Si kwa ajili ya kwenda kufanya siasa pekee. Nia yangu kubwa ilikuwa kufika nyumbani kwetu kuwajulia hali wazazi wangu. Akiba yangu ya pesa haikuwa ndogo. Ningeweza kabisa kuwajengea nyumba bora zaidi, kuwanunulia mavazi mapya na kumpatia baba baiskeli. Nilimwambia hivyo Mpare. Lakini alinicheka tena kabla ya kuniuliza, “Baada ya kujenga hiyo nyumba?”


Sikumjibu haraka. Akaamua kujibu kwa niaba yangu. “Baada ya nyumba utarudia kwenye umasikini wako. Hutakuwa na kitu tena. Kwa maana hiyo ni kwamba huna kitu. Lazima tutafute pesa zilizotakata. Achana na vijisenti ambavyo havitabadili maisha yako.”


Ndipo nikamwomba aache nilifikirie wazo lake hadi kesho, fikra ambazo zilifanya nipoteze usingizi wangu kucha na kubakia nikitapatapa kitandani kuubembeleza.


Nilishawishika.




* * *?


Kuwinda sio lelemama. Sio kuingia porini, kuona mnyama, kuelekeza bunduki na kuifyatua peke yake. Ni zaidi ya hapo. Kuwinda kuna miiko na maadili yake. Mimi sikuwa




mwindaji. Lakini sehemu kubwa ya maisha yangu nikiwa nimeitumia maporini nilikuwa nimeona mengi na nimejifunza mengi, mengi tosha kunipa ujanja na maadili ya porini.

Kwa mfano, usiku mmoja tukiwa katika barabara moja mbovu, ya mkato katika maeneo ya Makuyuni, nilishangaa kuona njia imeziba ghafla. Nikasimamisha gari na kumuuliza mmoja wa abiria wangu kuna nini mbele yetu. Aliangalia mara moja tu na kuniambia “Tembo.”

Kumbe tembo mkubwa alikuwa amesimama katikati ya njia akitutazama. Baada ya muda alianza kutusogelea taratibu. Nikaweka gia ya kurudi nyuma na kuanza kurudisha gari taratibu. Tembo alizidi kutusogelea. Kwa wasiwasi nilijikuta nimerudisha gari vibaya na kuingia shimoni. Tembo aliendelea kuja taratibu. Mara nikamsikia abiria wangu mwingine akiuliza kama kulikuwa na mtu mwenye kiberiti. Nilikuwa nacho. Nikampa. Kwa mshangao wangu alishuka nje ya gari na kuwasha sigara. Moshi na harufu ya sigara ulipeperushwa na upepo kuelekea aliko tembo, tulimwona akisita. Kisha tembo yule aligeuka na kuondoka zake taratibu kama alivyokuwa akija.

Tembo hapendi harufu ya sigara.

Katika tukio jingine niliwahi kulala ndani ya hema langu mapumzikoni, huko Ngorongoro. Nyakati za alfajiri nilipata hisia kuwa mambo si shwari. Nikafungua macho kutazama nje. Pazia la hema langu lilikuwa limefunguka. Simba wawili, dume na jike waliketi pale mlangoni wakinitazama. Walipoyaona macho yangu waliinuka na kuondoka zao polepole. Niliwatazama hadi walipotokomea porini.

Wanyamawanajuabinadamunidhaifu,hawamshambulii bila sababu.




Nilimsimulia hayo Mbonea. Hayo na mengine mengi. Nilimwambia kimaadili ni mwiko kumuua mnyama mwenye mtoto au watoto.

“Hutakuwa umeua mnyama mmoja tu, bali wengi. Baadhi ya wanyama wachanga huweza kutembea dakika tatu tu baada ya kuzaliwa. Wanamhitaji mama kwa maziwa na ulinzi. Ukimwua mama umewaua wao pia,” nilimfafanulia.

“Binadamu tunamwogopa sana simba, pengine na chui,” nilimweleza. “Lakini wanyama wote ni hatari. Nyati, kwa mfano, ni mnyama mwenye hasira na hila nyingi. Ukimpiga risasi ukamwona ameanguka usije ukamsogela. Wakati mwingine hata ukiwa umemkosa au kumjeruhi atajiangusha chali na kujifanya kafa. Ukimsogelea unakufa wewe. Kifo cha nyati ni mpaka pale utakapoona amejikojolea.”

“Mkojo huo wa nyati akiwa hai ni silaha kali sana.” Niliongeza. “Kama utakuwa umepambana na nyati halafu unamkimbia na kupanda juu ya mti atakachofanya ni kuukojolea mkia wake na kisha kurushia mkojo huko aliko. Mkojo wake unawasha sana. Ukikupata kwa vyovyote utaachia mti na kuanguka chini, ambako utamkuta akikusubiri. Atakusagasaga kwa miguu na pembe zake hadi ahakikishe umekufa.

Mpare Mbonea alishangaa. Ilikuwa dhahiri kuwa hilo hakulijua.

“Tembo hata kama hujampiga risasi, ukimwona kaanguka usimwogope. Tembo akianguka haamki, huwa ndio mwisho wa maisha yake. Ndiyo maana tembo hata akilala hulala wima, ama kwa kujiegemeza kwenye mti au kwa tembo wawili kuegemeana.”

Hilo pia Mbone hakulijibu. Alizidi kuduwaa.






“Huyu tunayemwinda ni mkali zaidi na wa hatari zaidi,” niliongeza. “Kwa bahati hana akili nyingi. Kifaru ana nguvu nyingi sana na kasi ya ajabu. Akikuona unatishia maisha yake atainama na kukujia kwa kasi, macho kayafumba, kwa lengo la kukuchoma lile pembe lake. Ukiona hivyo ondoka haraka sana eneo hilo. Wawindaji wajanja hulipata pembe lake kirahisi sana kwa njia hiyo. Wao husimama mbele ya mti mkubwa. Faru anapokuja huondoka mara moja kwa hasira zake na hujikuta amechomeka pembe lake katika shina la mti huo na kulididimiza. Katika jitihada za kuitoa mara nyingi pembe hiyo hung’oka, kifaru hutokwa na damu nyingi na baadaye kukata roho.


Mwindaji hujipatia hitaji lake kwa urahisi kabisa.” Mbonea alinisikiliza kwa makini sana, kana kwamba nilikuwa nikimfundisha namna ya kuingia katika ufalme wa mbinguni. Alinisikiliza. Lakini sina hakika kama alikuwa akinisikia, kwani mara alipopata nafasi ya kwanza aliivunja kanuni ya kwanza kabisa ya uwindaji. Kitendo hicho kiliniua kwa mara ya pili katika maisha yangu.



SURA YA KUMI NA TISA?

Pembe Za Faru?



W

anasema ‘za mwizi arobaini’. Sisi hatukuzihitaji arobaini hizo. Siku ya tatu tu, toka tulipoanza shughuli hizo, ilitosha kabisa

kututia hatiani.

Tukio hilo lilianza hivi;

Baada ya kufika na Mbonea, aliniacha Arusha na kwenda Kilimanjaro. Aliporejea jioni hiyohiyo, akiwa na ‘vifaa’ vyake; viatu aina ya safari, suruali na shati la kaki, mfuko wa ngozi na zaidi ya yote silaha. Alikuwa na bunduki kuukuu ambayo aliielezea kama hazina yake pekee itakayomtoa katika lindi la umasikini. “Hii ndio baba, ndio mama. Nina hakika haitaniangusha,” alisema wakati akiitoa katika mfuko wake na kunikabidhi ili niikague.

Alfajiri ya siku iliyofuata tuliuacha mji wa Arusha, tukiifuata barabara ya Dodoma. Tulivipita vitongoji vya Ngarenaro, Sombetini na Majengo. Tukafika Kisongo na kuiacha njia ya Monduli kulia hadi tulipofika Makuyuni. Hao tungeweza kuelekea kulia vilevile na kufika Mto wa Mbu, Karatu na hatimaye Ngorongoro ambako nilitarajia tuanzie shughuli zetu. Tulipita kwa chini na kuliona ziwa Manyara kwa mbali kabla ya kuingia Magugu na hatimaye Babati.




Mbonea alisisitiza sana juu ya kuwatafuta vifaru kabla ya wanyama wengine. “Pembe zao ni almasi!” “Zinatafutwa sehemu mbalimbali za dunia.” Tukiipata walao moja tu….”

Nilitamani kucheka. Kwangu mimi kifaru ni mnyama mwenye sura mbaya na umbile lisilovutia kuliko wanyama wengine wote. Alivyokuwa na bahati mbaya zaidi pembe zake hizo kubwa na ndogo, zinazodaiwa kuwa za thamani zimeota juu ya pua, katikati ya uso wake. Wataalamu wanasema pembe hiyo ni mkusanyiko wa aina fulani ya nywele, zinazoota toka kwenye fuvu lake la kichwa jambo ambalo hupelekea kupoteza pembe hizo apoteze pia uhai wake.

Mbonea alinisikiliza kwa shahuku. Lakini nilihisi shahuku yake kubwa ilikuwa ni kumwona kifaru na kumpiga risasi, si vinginevyo.


* * *?

Kifaru anaweza kuishi kati ya miaka 35 hadi 40, umri ambao humwezesha kufikia uzito wa tani moja na nusu hadi mbili. Pamoja na uzito huo anaposhambuliwa hukimbia kwa kasi kati ya kilomita arobaini na tano au hamsini kwa saa. Kifaru hana makuu. Pamoja na machachari yake yote chakula chake pekee ni majani, hata yale yenye miiba. Si msumbufu, kwani muda mwingi wa mchana hupenda kujipumzisha kando ya mito au mabwawa. Hali hiyo hufanya kazi ya kumwinda isiwe ngumu kama inavyotarajiwa.

Imani ya muda mrefu juu ya pembe zake hizo, kuwa hutengeneza dawa fulanifulani muhimu kwa binadamu pamoja na mapambo murua ni sababu iliyofanya aanze kuadimika sana duniani. Ukweli huo niliufahamu fika kupitia matangazo ya watetezi wa wanyama katika vyombo vya habari. Na hivyo






ikawa sababu mojawapo iliyonifanya kushiriki katika jukumu hili huku roho ikinisuta.


Lakini pindi maji ukishayavulia nguo huna budi kuyaoga. Sikuona kama ingekuwa uugwana kubadili uamuzi, hasa nikiwa tayari humo porini. Nilimwelekeza Mbonea maeneo yote ambayo yalikuwa na sifa za kuishi vifaru. Nilimkumbusha mara kwa mara kuwa makini. “Macho ya kifaru ni dhaifu kidogo kuona mchana. Lakini pua zake ni makini sana. Akipata harufu yako kabla hujamwona na akishuku kuwa una nia mbaya ujue kuwa utakufa wewe badala yake,” nilimwambia.


Nikaongeza, “Lakini kifaru si wa kuogopa zaidi. Yupo askari wake. Huyu ni ndege ambaye muda wote hukaa juu ya miili ya vifaru akidonoa wadudu wanaomsumbua. Wakati mwingine hata pale kifaru anapokuwa na jeraha ndege hawa huliongeza kwa kulidonoadonoa. Kifaru humvumilia. Pengine analazimika kumvumilia kwa kuwa hana la kufanya. Ndege huyo huona mbali sana na humshtua kifaru kwa mlio wake mara anapohisi dalili za hatari kwa bosi wake.”


Wataalamu wanakubaliana kuwa Ngorongoro ni moja ya miujiza kadhaa ya dunia. Wanaikadiria kuwa ni mwujiza wa nane duniani. Miujiza mingine ikiwa pamoja na ile ya yale majengo yaliyopo Misri. Piramidi, ambayo yalijengwa miaka ipatayo 4700 iliyopita lakini yangali hai hadi leo. Mojawapo ambayo yametumia mawe na miamba yenye uzio wa tani moja hadi mbili kila moja na kupaa juu urefu wa meta 140. Ikizingatiwa kuwa wakati huo hakukuwa na vifaa maalumu vya ujenzi kama leo, majengo hayo yaliyoandaliwa kama hifadhi ya miili ya farao yanamshangaza kila mtu anayeyaona. Sanamu ya mmoja wa miungu ya wagiriki, Zeus, akiwa amekaa juu ya kiti chake cha enzi, chenye ukubwa wa meta 12, ikiwa




imeundwa kwa meno ya tembo na kupambwa aina mbalimbali za madini ni mwujiza mwingine wa dunia.

Muujiza wa Ngorongoro unatokana na maumbile yake. Wakati eneo hili ambalo limo katika Bonde la Ufa linakadiriwa kuwa na ukubwa wa kilometa za mraba 8,300 zenye wanyama pori wapatao 300,0000 ndani ya eneo hilo kuna kilometa za mraba zipatazo 250 za kushangaza ziadi. Eneo hili, katika mabadiliko mbalimbali ya maumbile ya dunia lilididimia kwa kiasi cha meta 600 toka usawa wa ardhi. Humo ni shamba pekee la wanyama. Zaidi ya wanyama wapatao 20,000 wakiwemo vifaru weusi, nyati , pundamilia, tembo, fisi na wanyama wengine tele. Wamo pia ndege anuai na wadudu.

Ikiwa kama bustani ya aina yake, eneo hilo lenye maji tele, lishe ya kutosha na mazingira ya kuvutia limefanywa na wanyama hao kama makazi yao ya kudumu ingawa wanao uwezo wa kutoka na kuingia.

Kama ambavyo eneo hili humshangaza kila binadamu anayeliona kwa mara ya kwanza ndivyo lilivyomshangaza rafiki yangu Mbonea. Nilihisi kuona kitu kama machozi yakimlengalenga katika macho yake na dalili za udenda kumtoka pale tulipoingia na kuwaona wanyama mbalimbali wakiendelea na shughuli zao bila ya kututilia maanani. Twiga mmoja aliyekuwa akinyonyesha aligeuka kutuangalia kidogo kisha akaendelea kula juu ya kilele cha mti. Swala mmoja alikurupuka toka kichakani na kukimbia hatua kadhaa kabla hajasimama, kututazama kwa muda kabla na kisha kutokomea tena vichakani. Kwa mbali sana, tuliweza kuona kundi kubwa la nyati likipunga upepo huku vitoto yao vikiruka huku na huko katika michezo yao ya kawaida.

Mbonea alizidi kushangaa. Alishindwa kustahimili,




chozi likamdondoka. Alijaribu kulifuta harakaharaka, lakini haikuwa kabla ya kuliona, jambo lililofanya niangue kicheko. “Tunawatafuta faru,” nilimkubusha. “Sio kitoweo. Kwa hiyo, punguza papara.”

Tulizurura maporini humo kwa siku nzima. Tulipita katika mito ya layara, oljiro na Mungo. Tulipita kandokando mwa ziwa Makkat na katika bwawa la Mandus. Tuliingia hata katika msitu wa Lerai. Tuliwaona wanyama wengi sana isipokuwa yule tuliyemwitaji, kifaru. Ilikuwa siku mbaya.

Siku ya pili ilianza kwa namna ya pekee. Ilikuwa angavu sana na hata hali ya hewa haikuwa ya ubaridi mkali. Tulifuata barabara ya Lemaka iliyotupeleka tena kwenye ziwa Makkat ambako tulikuwa tumeona dalili za wanyama hao vikiwemo kinyesi na nyayo. Wakati tukiwa umbali wa kilometa moja toka ziwani hapa nilisikia milio ya ndege, askari wa vifaru ikitokea vichakani. Kisha niliwaona ndege hao wakiruka angani na kutokomea.

“Wapo,” nilimwambia Mbonea. “Kwa bahati mbaya, wameshapata hisia za hatari. Lazima tuwe waangalifu sana,” nilimsisitizia. Hata hivyo, nilikuwa na mshangao kidogo. Ndege hao walikuwa wametuona sisi kweli au hatari nyingine? Maana tulikuwa mbali na pale walipotokea.

Tulitembea kwa hadhari kuelekea huko, mitutu ya bunduki zetu ikiwa imeelekezwa mbele, tayari kufyatuliwa iwapo lingetokea lolote lile. Tulipofika pwani ya ziwa tuliambaa nayo kuelekea upande wa kulia walikorukia ndege. Hata kabla hatujapiga hatua ishirini tulimwona kifaru mmoja akiwa amesimama katika hali ya tahadhari akiangalia tunakotokea. Alikuwa na mtoto, kifaru mdogo ambaye alisimama katikati ya miguu ya mtoto wake.




Mara nikamwona Mbonea akipiga goti chini na kulenga shabaha. “Usimwue… ananyonyesha…” nilijaribu kumwambia. Sauti yangu ikimezwa na mlio mkubwa wa ghafla kutoka kwenye bunduki yake. Alikuwa na shabaha ya pekee. Risasi ilipenya katika paji la uso la kifaru huyo bila kuharibu pembe zake. Kifaru alitapatapa kwa muda akipigania roho yake kabla hajaanguka chini. Risasi ya pili, iliyomwingia tumboni ilimfanya akate roho palepale.

“Umefanya nini?” nilimuuliza kwa ukali. “Nilikuonya mapema kuwa mnyama anayenyonyesha! Kinda yule atafanya nini peke yake katika mazingira haya?”

Mbonea alikuwa akitabasamu, tabasamu pana ambalo sikupata kuliona huko mbeleni katika uso wake. Badala ya kunijibu nilimsikia akisema, “Mmoja tayari! Bado wawili tu tumekuwa matajiri!”

Nilikuwa nimekasirika kiasi kwamba nilitamani kumlenga bunduki yangu na kuifyatua. Majuzi tu alikuwa akilalamika watoto wake pacha waliopoteza maisha kwa utapiamlo leo anaacha mtoto wa faru apoteze maisha kwa njaa, baridi au kukosa kiongozi wa kumsaidia mbinu za kuishi porini.

Mbonea alijua nimekasirika. Hakujua kama alinikasirisha zaidi pale aliposema “Toto la kifaru litakufaa nini rafiki yangu. Hata pembe halina. Achana nalo, tushughulikie mali yetu.”

Wakati huo ‘toto’ hilo la kifaru lilikuwa limehisi kuwepo kwa jambo baya lililomtokea mama yake. Lilionyesha kushangazwa na damu. Likamzunguka mama yake mara tatu na kujaribu kumtikisa kabla halijaanza kulia kwa sauti yake mbaya, sauti ambayo masikioni mwangu ilitia huzuni kubwa.



Sijui nini ambacho kingefuata baina yangu na rafiki yangu Mpare kama jambo jingine, kubwa zaidi, lisingetokea. Tulijikuta ghafla tumezingirwa na kundi la askari wa wanyama pori wasiopungua sita, kila mmoja akiwa na bunduki mkononi. Na kila bunduki ikiwa imetuelekea.

“Tueni bunduki zenu chini na muweke mikono yenu juu mara moja!” mmoja wao alitoa amri.

Tulitazamana na Mbonea kwa mshangao. Hatukuwa na namna yoyote ya kupambana nao wala kukimbia. Tukaziangusha bunduki na kuweka mikono yetu juu ya vichwa.

“Washenzi wakubwa nyie,” askari yule aliendelea kufoka. “Tumemlinda kifaru huyu kwa miaka nyie mnamuua kama mchezo. Mtakuwa mfano mzuri sana kwa jamii. Kama hamjafungwa maisha, miaka ishirini kwa kila mmoja wenu haitamkosa.”

Walizichukua bunduki zetu. Wakatutia pingu za mikono kisha tukaanza kusukumwa kuelekea walikoificha gari yao. Tukatupwa ndani ya gari, ikatiwa moto na kuelekezwa mjini Ngorongoro ambako tulifungiwa katika kijichumba kidogo kwa siku tatu kabla ya kupelekwa Arusha. Tulifunguliwa mashataka.


* * *?

Kabla ya kesi yetu kuanza kusikilizwa tulikaa rumande kwa wiki tatu nzima, tukiwa tumewekwa katika chumba cha watu hatari sana. Chumba hicho kilijumuisha watu watatu wa kesi za mauaji, watu watano wanaotuhumiwa kwa kujaribu kuvunja benki kwa nia ya kuiba, mmoja aliyekamatwa akimnajisi ng’ombe na wengine tele wenye tuhuma hii au ile.




Mmoja kati ya watuhumiwa hao nadhani alikuwa kichaa. Siku zote , wakati wote, alikuwa mtu wa kupiga kelele. Na kauli yake ilikuwa moja tu; ‘Nitaua mtu. Kama si leo kesho!’ Kauli hiyo ilinitisha sana kwani sikujua alikusudia kumwua nani. Hakimu anayesikiliza kesi yake, askari aliyemkamata au yeyote kati yetu mahabusu wenzake. Macho yake yalikuwa yanatisha, sura yake ikitangaza shari kama shetani mwenyewe. Kwa kweli alininyima raha na kufanya nijitahidi kila ilivyowezekana kumkalia mbali.

Hiyo ndiyo jumuiya mpya niliyojiunga nayo, jumuiya ya wahalifu, jumuiya ya waasi wa sheria. Mimi, Petro Mtukwao Kionambali Kalimanzira tayari nilikuwa mmoja wao. Machoni mwa jamii nilikuwa mtu duni, asiyefaa kuishi uraiani bali gerezani kusubiri hukumu kamili.

Ilinisikitisha zaidi pale watuhumiwa hao walipotupokea kwa furaha kana kwamba sisi ni mashujaa. “Jengo hili limejengwa kwa ajili ya wanaume kama nyie,” mmoja wao alisema. “Bila nyie, polisi na mahakimu wangekufa njaa, kwani hakuna mtu ambaye angekubali kuwalipa mishahara bure!”

Sikumwelewa.

Wala hakunijali. Aliendelea na mawaidha yake ya kishetani, “Wanaletwa hapa watu kwa makosa ya kitoto kabisa. Eti jitu zima limepiga hadi kumwua mkewe au mwanawe. Eti jitu na akili zake limeiba kuku wa jirani. Nyie wanaume bwana! Kuingia msituni, kupambana na wanyama hatari kama faru ili mpate zile pembe zake ni uanaume. Kukamatwa kwenu ni ajali kazini tu. Kama msingeshikwa mngekuwa matajiri wakubwa kutoka nchi hii.”

Hiyo ndiyo jela! Hakuna siri! Toka siku ya kwanza tulipoingia tayari tulikuwa gumzo. Kila mmoja alionyesha dalili




ya kutupongeza! Laiti wangejua nilivyokuwa najisikia moyoni! Nilikuwa taabani kwa aibu na kukosa raha. Sikutegemea kamwe maishani nifanye kitendo chochote, ama kwa makusudi ama kwa bahati mbaya, ambacho kingeniweka upande wa pili wa sheria. Nilikuwa na nilitegemea kuwa mtu mwaminifu na mwadilifu katika uhai wangu wote. Nilijuta kukutana na Mbonea. Nilijuta zaidi kumsikiliza. Nilitamani kumchukia maisha yangu yote. Nilitamani kumwambia hayo.

Hata hivyo, Mbonea hakuwa katika hali ya kuambiwa hayo. Toka tulipokamatwa muda wote alikuwa mtu wa kutokwa machozi. Mara nyingi, kwa sauti inayotetemeka, nilimsikia akinong’ona, “Bibi yangu kikongwe atafanya nini jamani… dada yangu kiwete ataishi vipi…” alisema huku akifuta machozi. Kwa muda huo mfupi Mbonea tayari alikuwa amekonda na kupungua uzito kwa zaidi ya kilo kumi. Hakupata usingizi. Alikula kwa shida baada ya ushawishi mwingi. Ndiyo, ni yeye aliyeniingiza katika mkasa huo. Lakini kwa jinsi alivyokuwa akitia huruma nilijikuta nikimhurumia kuliko hata nilivyojihurumia mimi.

Mbonea alikuwa na ndugu wengi. Alitembelewa na watu mara kwa mara na kujadiliana nao hili na lile. Nilishangaa alivyokuwa haonyeshi nia ya kunishirikisha katika maongezi hayo, ambayo nilitarajia yangelenga katika kutafuta ufumbuzi wa tatizo letu. Sikuwa na la kufanya. Nikabakia na uyatima wangu nikiyaweka yote mikononi mwa Muumba.

Kabla ya kupelekwa mahakamani, tulihojiwa na watu mbalimbali, polisi, wanasheria na hata watuhumiwa wenzetu. Kila mmoja alikuwa na ushauri wake kwetu. Polisi na wanasheria wa serikali walinishauri kukiri kosa ili kupunguza uzito wa adhabu. Wanasheria wengine walinishauri kukataa



katakata kuhusika na suala hilo. Watuhumiwa na wenye uzoefu wa masuala ya kesi pia walinionya juu ya athari za kukubali kosa kubwa kama lile. Hali iliyofanya nijione kuwa nachangwanywa akili.

Tatizo jingine lilikuwa mshitakiwa mwenzangu. Kila nilipomtaka tukae na kuweka mkakati wa pamoja alikuwa akiishia kulia tu. Hatukupata hata mara moja kukaa na kuzungumza lolote kwa tuo. Mbaya zaidi ni pale ambapo tulikuwa tukihojiwa na hata kuandika maelezo kila mmoja kwa wakati wake. Sikujua amejieleza vipi na kuandikisha lipi, kama ambavyo niliamini yeye hakujua nilichoeleza.

Hatimaye, siku ya siku ikafika. Tulichukuliwa na lori la polisi toka gereza la Kilimwanga, tulilokuwemo na kupelekwa mahakamani mjini Arusha. “Pilato” alikuwa mzungu, mtu mfupi; mwembamba mwenye sura ya kitoto. Isipokuwa kwa miwani mizito na joho alilovaa isingekuwa rahisi kumfananisha na hakimu. Nilikuwa nimepata sifa nyingi za hakimu huko gerezani. Nusu ya wafungwa wote ni yeye aliyewahukumu. Nilikwishaambiwa mapema kuwa kama tungemkuta hakimu huyo, ambaye gerezani walimwita “Fisi maji” kwa ukali wake, gereza lisingeweza kutuepuka. Ajabu ni kwamba kwa sura hakuonekana katili kama alivyoelezewa.

Siku hiyo mahakama ilikuwa na kesi nyingi, kubwa na ndogo. Lakini nadhani kesi yetu ndiyo iliyomvutia zaidi maana niliona kesi nyingi akiziendesha harakaharaka. Zingine alizihairisha na nyingi alizitolea hukumu bila umakini mkubwa, huku mara kwa mara akitupa jicho upande wetu kama anayetusubiri kwa hamu.

Saa na hatimaye dakika ikawadia. Tukiitwa kwa majina, mmoja baada ya mwingine na kusimamishwa kizimbani. Mimi




nikitetemeka kidogo, mwenzangu akitetemeka na kupepesuka kama jani la mwembe.

Hakimu alivua miwani na kututazama kwa takribani dakika nzima, kabla hajaivaa tena na kusoma jalada la tuhuma zetu lililokuwa mbele yetu. “Petro Mtukwao Kionambali… Daniel Mbonea mnashtakiwa kwa kuingia katika hifadhi ya taifa ya Ngorongoro kwa makusudi ya kufanya vitendo vya uharamia. Kosa la pili, kwa makusudi vilevile mlimuua mnyama aitwaye kifaru kwa kumpiga huku mkijua fika kuwa kifaru huyo ni mmoja wa wale wanaolindwa na serikali kwa gharama kubwa ili kuifadhi viumbe hao walio hatarini kutoweka. Aidha, kosa lenu la tatu ni kumwua kifaru huyo huku mkijua na kuona wazi kuwa alikuwa na mtoto mchanga ambaye alimtegemea. Kwa maana hiyo mmehatarisha maisha ya kichanga huyo pia.” Hakimu alivua tena miwani yake na kunikazia macho,?

“Petro Mtukwao Kionambali… ni kweli au si kweli?”

Nikageuka kumtazama mwenzangu. Alikuwa akinitazama pia, ingawa macho yake yalijaa machozi. Kwa namna fulani alikuwa kama anayenisihi jambo fulani. Sikujua ni jambo lipi. Nikainuka na kumtazama hakimu. “Ni kweli Mheshimiwa,” nilijibu.

Nilipata hisia kuwa kila mtu katika chumba hicho cha mahakama, ikiwa pamoja na hakimu mwenyewe, alipigwa na butwaa. Hakimu aliinama, akaandika jambo katika faili lake, kisha akainua tena miwani na kumkazia macho Mbonea. “Daniel Mbonea, mashtaka haya ni kweli au si kweli?”

“Sio kweli, Mheshimiwa,” Mbonea alijibu kwa sauti iliyokuwa na uhakika kinyume na hali yake.

Hakimu aliandika jambo. Akainua tena uso wake na kututazama kwa zamu kabla hajauliza, “Nataka kufahamu




kitu kimoja. Kati yenu nani aliyefyatua bunduki, ambayo risasi yake ilimuua kifaru yule?”

Tulitazamana tena na Mbonea. Alikuwa amebadilika tena. Anatetemeka na anapepesuka nusura aanguke chini. Macho yake yalijaa huruma na simanzi. Niliweza kuyasoma mawazo yake katika macho yake hayo; bibi yangu kikongwe atafanya nini jamani… dada yangu kiwete ataishi vipi… ujumbe ambao ulinifikia bila sauti. Ukanitia huruma. Bila kujua nilifanyalo, niliinua tena mkono wangu na kumjibu hakimu, “Ni mimi Mheshimiwa.”

Nilisikia sauti za kitu kama, “Ah!” zikiwatoka watu wawili watatu chumbani humo. Wengi wao walinikazia macho ya mshangao na kutoyaamini masikio yao. Hata hakimu alionekana kutoamini kile alichokisikia. Akaandika alichokuwa akikiandika. Kisha aliahirisha kesi kwa kupanga tarehe ya hukumu.

Tukarudishwa mahabusu. Huko nilikuwa gumzo kubwa. Kila mtu aliyesikia kilichotokea mahakamani alitaka kuniona kwa macho na kuisikia sauti yangu.

“Pole sana, mdogo wangu,” mzee mmoja aliyekaa rumande kwa miaka tisa sasa aliniambia. “Hivi hujaambiwa kuwa hata kukubali kosa ni kosa? Maana yake ni kwamba ulifanya kosa huku ukijua kuwa unafanya kosa. Adhabu yake ni kubwa sana. Humu, wewe anza kutafuta kona yako ambapo utalala kwa miaka ishirini. Halafu huonekani kama mtu wa kumudu chawa, kunguni na chakula cha ajabu kinachotolewa.” Nadhani nilikuwa nimechanganyikiwa kwani haikuniingia akilini uzito wa mkasa uliokuwa mbele yangu hadi siku ya hukumu. Hakimu, akiwa mkali kama pilipili, alitumia zaidi ya dakika arobaini kuelezea athari za ujangili?



kwa wanyamapori hasa wale adimu kama faru. Alitoa mifano ya nchi mbalimbali za dunia ambazo zimeweka sheria kwa ajili ya kuwalinda wanyama ambao wanazidi kutoweka siku baada ya siku.

“Tumeirithi nchi hii ikiwa na mazingira murua, wanyama na ndege tele. Tumerithi hayo kwa kuwa babu zetu hawakuwa waharibifu wala katili kwa wanyama. Tunahitaji watoto na wajukuu zetu nao warithi hali ile tuliyoikuta. Kwa bahati mbaya baadhi yetu wametia pamba masikioni mwao. Wanapuuza jitihada zote za serikali na dunia kwa matarajio ya maslahi yao binafsi. Hawa lazima wawe mfano kwa wengine kwa kupewa adhabu kali,” hakimu alisema.

“Kesi iliyo mbele yangu inamhusu Petro Mtukwao Kionambali na Daniel Mbonea. Hawa walikamatwa na askari wa wanyamapori waliokuwa wakitelekeza jukumu lao la kumlinda kifaru huyu mwenye mtoto. Kwa ukatili mkubwa walimpiga risasi na kumwua.”

“Katika maelezo yao hapa mahakamani na hata yale ya awali, Mbonea alikataa kuhusika na mauji haya. Anasema kuwa alimtembelea rafiki yake huyo mbugani baada ya kufahamiana naye mjini Moshi na Arusha bila kujua kuwa kazi yake ni uwindaji wa vifaru. Kuwa kifaru yule mwenye mtoto alipotokea alimwona akiandaa bunduki na kutaka kumwua. Alimtahadharisha lakini Kionambali hakumsikiliza. Alifyatua risasi na kumwua kifaru yule. Kwa upande wake Kionambali mwenyewe katika maandishi na maelezo ya ana kwa ana mahakamani amekiri yote yaliyotokea. Hivyo, mahakama inamwachia huru Daniel Mbonea. Aidha, inamuhukumu Petro Mtukwao kifungo cha kwenda jela miaka ishirini na kazi ngumu na viboko kumi, ili awe mfano kwa wengine.”




Sikuelewa. Nilimwona Mbonea akibebwa juujuu na ndugu zake huku wakishangilia. Mimi nilitiwa pingu, nikasukumwa kuelekea kwenye gari la magereza ambako nilipandishwa na kurejeshwa Kilimanga ambako nilivuliwa mavazi ya uraiani na kuvishwa yale ya gereza yenye namba na tarehe yangu ya kufunguliwa. Niliondolewa katika chumba cha mahabusu na kuelekezwa katika selo nyingine ambayo ingekuwa makazi yangu hadi mwisho wa kifungo changu. Kama ile ya mahabusu hii pia haikuwa na kitanda wala godoro. Nilipewa blanketi kuukuu na kuelekezwa mahala pa kulala. Juu ya sakafu ngumu. Kona moja ilikuwa na kijichumba kidogo chenye harufu kali ambacho kilitumiwa kama choo na bafu. Mlikuwa na bomba lakini halikupata kutoa walao tone moja la maji!

Nilitoka nje na kuketi mahala fulani nikiwa nimejiinamia. “Pole sana,” nilisikia sauti ikiniambia. Nikatazama. Alikuwa yule mzee wa miaka tisa mahabusu. “Nilikuuliza kama unamwamini mshtakiwa mwenzako hukupata kunijibu,” alisema na kuendelea, “Yule kakuuza rafiki yangu. Kesi yenu ilikuwa mbaya sana. Ilikuwa lazima mtu afungwe. Amekuchezea akili umefungwa wewe, yeye ametoka.”

“Kwa vipi?” niliuliza “Mbona mtu mwenyewe alikuwa mtu wa kulialia muda wote?”

“Kulia!” mzee alisema akicheka. “Kama alikuwa analia kweli basi yalikuwa machozi ya mamba. Alikuwa akikuchota akili huku akikucheka. Kwa bahati mbaya, wewe ulishiriki kumrahisishia azma yake kwa kukiri hili na lile. Hilo limemfanya atoke haraka kuliko alivyotegemea.”

Machozi ya mamba! Niliwaza kwa mshangao.


?

20

Ben R. Mtobwa












SURA ISHIRINI?

miaka ishirini



M

fikiriemtotomdogosanawakiume, aliyeondoka kwao zamani sana kuiokoa roho yake, mtoto ambaye alifuatana na babu yake, wakavuka

misitu na nyika, milima na mabonde, mito na mabwawa hadi nchi ya mbali. Huko mtoto aliona nuru mpya elimu. Akaanza kusoma huku akiwa na matumaini.

Mtoto huyu, ambaye kwa miaka nenda miaka rudi alikuwa hajazitia machoni sura za wazazi wake wapenzi, wala kuonana na babu yake kipenzi, majuzi tu alikwishafikia uamuzi wa kurejea nyumbani. Na alitarajia kupokelewa kishujaa kwani akiba yake benki ilikuwa ya kuridhisha. Angeweza kujenga nyumba ya kisasa na kutoa zawadi nyingine tele ambazo zingefanya ukoo mzima umshangilie. Lakini, kwa mara nyingine tena likatokea jambo jingine, kubwa kuliko yote yaliyopata kutokea. Na sasa yuko kifungoni. Hategemei kutoka kabla ya miaka ishirini! Hategemei kuwakuta wazazi wake wakiwa hai! Yeye mwenyewe hategemei kutoka akiwa hai!

Mtoto huyo ni mimi, Petro Mtukwao Kionambali. Tayari miezi miwili ilikuwa imepita toka nianze kutumikia kifungo. Miezi miwili! Ilibakia miezi isiyopungua mia mbili thelathini na nane, nikiwa ndani ya chumba hiki kinachonuka, nikilala juu






ya sakafu hili gumu na kula chakula chao kisikolika! Mara kwa mara wafungwa wenzangu walinishauri nijitahidi kuyazoea maisha ya jela, lakini yalikuwa hayazoeleki. Binadamu gani atazoea kula mlo mmoja, tena usioridhisha, kwa siku? Binadamu gani atazoea kula saa kumi na moja jioni, katika chumba kisicho na madirisha na kutoipata tena hewa ya nje hadi kesho yake?

Niliteseka sana kialikili zaidi ya kimwili. Nilitafakari kwa nguvu zangu zote na kushindwa kabisa kutambua kitu gani kinafanya siku zote niwe kondoo wa kafara. Sikuweza kuelewa kwa nini nilikwenda Kilimanjaro na kukutana na ‘Mpare’ Daniel Mbonea. Sikuweza kuelewa kwa nini nilikubali kushawishika hata nikafuata ushauri wake na kuahirisha dhamira yangu ya kurejea nyumbani Buha na badala yake kuingia naye porini kuwinda nyara za serikali. Zaidi sikuweza kuelewa kabisa sababu iliyofanya nijisikie kumhurumia kiasi cha kumlinda kwa kujitoa kuwa ni mimi niliyefyatua risasi ya kumwua kifaru kutokana na madai yake ya kutegemewa na bibi kizee na dada kiwete? Mie pia si nilikuwa na babu kizee na ndugu vilema wengi tu ambao walinitegemea. Machozi yake ya mara kwa mara? Mie pia ningeweza kutokwa na machozi siku nzima kama ningependa. Kwa kweli sikuweza kabisa kuelewa sababu.

Hisia za siku nyingi, ambazo nilianza kuzisahau zilinirejea. Hirizi iliyopotea! Nilianza kueleka kuamini kuwa chanzo cha balaa na mikosi yangu ni kuipoteza hirizi ile ambayo babu alinihusia kuitunza. Una alama… alama ya shari... Niliyakumbuka tena maneno niliyoambiwa kule Sumbawanga na Mbeya. Pengine ni kweli? Pengine alama hii ndiyo iliyomvuta Mbonea? Iwe kweli iwe uongo, niliwaza,




kwa vyovyote vile ilihusiana na hirizi yangu iliyopotea. Kama ningekuwa nayo, niliendelea kuwaza, mtu yeyote mwenye nia mbaya nami asingenisogelea. Kamwe nisingewekwa alama!

Majuto ni mjukuu! Niliwaza. Nilikuwa na miaka isiyopungua ishirini ya kuishi katika gereza hilo huku nikiwaza hayo. Mawazo ambayo yangeweza kunitia kichaa. Lazima nijifunze kuachana nayo. Lazima nipate jambo jipya la kuwaza badala ya kukodolea macho kalenda nikiitafuta siku ambayo ingechapishwa baada ya miaka ishirini.

Nilijitahidi pia kumfukuza Mbonea katika fikra zangu. Bwana huyu alikuwa mtu wa ajabu sana. Alikuwa mnafiki asiye na haya kuliko binadamu wote niliopata kuwafahamu. Siku tatu tu baada ya yeye kupata uhuru wake na mimi kuanza kutumikia kifungo alikuja gerezani kuniona. Niliarifiwa kuwa nilikuwa na mgeni, sikuambiwa mgeni huyo alikuwa nani. Pengine nisingekwenda. Nikamkuta kakaa kitako akinisubiri. Alikuwa anang’ara mwili na mavazi, hali iliyofanya nijishuku kuwa nanuka jasho na uchafu wa nguo zangu.

Nilimwona akitafuta chozi la kunionyesha uchungu aliokuwa nao kwangu. Halikotoka. Sikuwa tena mgeni wa machozi yake ya mamba. Nilitamani kucheka. Hakunipa nafasi hiyo. Aliinuka na kunikumbatia bila ridhaa, kisha akanipa mkono wake wa kulia ambao muda wote alikuwa ameufumba. Nikaupokea na kubaini kuwa katika kunipa mkono huo alinipa kitu fulani kilichokuwa kiganjani. Nikaufungua mkono kutazama. Alikuwa amenipa kipande cha aina fulani ya jani.

“Nini hiki?” Nilimuuliza “Jani.”

“Jani la nini?”

“Jani la isale,” alinijibu.






Nililifahamu jani hilo. Isale ni majani uhimu sana kwa Wachaga. Hutumiwa kupanda katika mipaka ya mashamba, kuepusha migongano. Lakini jani hilo pia hutumiwa kwa upatanishi. Mchaga anapomfuata mwenzie kwa suala zito kama kuombana radhi, kudaiana na hata ndoa huweka jani hilo mkononi na kumshikisha mwenzi huyo kabla ya mazungumzo ya siri. Mara nyingi baada ya kitendo hicho mazungumzo huwa ya amani na mafanikio kwa pande zote mbili.


“Unanipa isale ya nini?” nilimuuliza.


“Nataka kukuomba radhi kwa yote yaliyotokea,” alisema. “Nataka tuendelee kuwa ndugu. Ndiyo, uko ndani niko nje. Nitautumia uhuru wangu huko nje kuhakikisha hukai ndani zaidi ya miezi mitatu. Nitahakikisha…”


“Umenipa isale ya nini?” nilimkatiza kwa ukali kidogo. “Mimi sio Mchaga na wewe sio Mchaga pia, kama ulikuwa ukisema ukweli.”


Mbonea alikohoa kidogo kabla hajanijibu akisema, “Ni kweli mimi sio Mchaga. Lakini sisi Wapare wa Ugweno tuna tamaduni nyingi zinazofanana na Wachaga. Moja ni jani hili. Tunalitumia katika upatanishi na mengineyo.”


Nilimtazama kwa makini mtu huyu. Alikuwa Mbonea yuleyule mwenye sumu ya nyoka na hila za kinyonga. Sikuona sababu za kuendelea kumsikiliza. Nikamwambia, “Sikiliza Mbonea. Mimi sio malaika. Mimi sio Yesu Kristo ambaye aliwaelekeza wanafunzi wake wakipigwa shavu moja wakinge na la pili. Mimi ni binadamu kama wewe. Naomba uondoke. Naomba usikanyage tena hapa kwa niaba yangu.”


Nadhaini hakunielewa. Nilimwona kaduwaa, hajui lipi zaidi aseme. Nilimwacha katika hali hiyo na kurudi katika ‘utumwa’ wangu wa miaka ishirini.




Siku mbili tatu baadaye nilipata ugeni mwingine. Huyu alikuwa mwanamke. Alikuwa mnene, maji ya kunde. Sura yake nzuri haikuwa na dalili zozote za dhiki wala misukosuko ya maisha. Alifuatana na watoto wawili wa miaka saba au minane, mapacha.

“Mgeni wangu?” Nilimuuliza. “Ndiyo. Wewe si Petro Kionambali?” “Ndiye.”

Basi mimi ni mgeni wako. Nimetumwa na rafiki yako Daniel Mbonea nikuletee chakula. Ameniagiza nikutembelee mara mbili kila wiki na kukuletea mahitaji yako yote muhimu.

“Mbonea!” Nikaropoka. “Wewe ni nani kwake?” “Mimi ni mkewe.”

Sikuyaamini masikio yangu, “Mkewe?” Nikauliza kuhakikisha. “Mke wa ngapi?”

“Kwani alikuambia anao wake wangapi?” “Ninachofahamu ni kwamba hana mke. Mkewe alifariki

zamani kwa kujinyonga.”

Ikawa zamu ya mama huyo kushangaa. “Mkewe alijinyonga?”

Kisha akaangua kicheko. “Bila shaka alikuwa akikutania. Tumeoana toka tukiwa vijana, sasa tunaelekea uzeeni. Hana mke mwingine, hana mke aliyepata kujinyonga.”?

Niliduwaa kwa muda. “Na hawa watoto? Unataka kuniambia kuwa ni wake?”

“Ndiyo. Ni watoto wetu. Alikuambia hana watoto?” Nilishindwa kumwambia kuwa kwa mujibu wa

Mbonea mwenyewe watoto wake pacha walikufa zamani kwa utapiamlo. Nilishindwa kuuliza juu ya bibi kizee na dada yake kiwete wanaomtegemea. Sikuhitaji kuhakikishiwa kuwa yote




aliyosema ulikuwa uongo, uongo mtupu, uongo uliokusudiwa kunitia huruma ili nishawishike kushirikiana naye katika dhamira yake chafu ya kutafuta utajiri.

“Mama, nashukuru sana,” nilimwambia. “Naomba umrudishie chakula chake. Halafu, tafadhali mwambie, sihitaji msaada wake wa aina yoyote si leo si kesho wala keshokutwa.”

Nikageuka na kuondoka zangu.

Nilimwacha mama huyo kaduwaa, haelewi kinachoendelea. Laiti angejua kuwa aliolewa na nyoka…


* * *

Gerezani kuna kiu. Kwangu kiu hiyo haikuwa ya vinywaji baridi au vinywaji laini. La, hasha! Ilikuwa kiu ya habari. Gerezani kuna njaa. Lakini njaa yangu mimi haikuwa ile ya chakula chao kibovu, ilikuwa ya kuona na kusikia kile kinachoendelea nje ya ukuta huo imara wa gereza la Kilimoanga. Kwangu hiyo ilikuwa adhabu kubwa zaidi na inayonitesa zaidi. Kwa nia ya kukidhi adha hiyo nilijenga urafiki na mfungwa mmoja kwa namna ya ajabu. Alikuwa na redio ndogo.

Kwa bahati mbaya, bwana huyu alipenda sana kusikiliza muziki. Mara kwa mara alitafuta stesheni zinazopiga muziki wa kina Mbaraka Mwinshehe na Salumu Abdallah. Nyimbo za ‘malaika’, ‘wanawake wa tanzania’, ‘mwanameka!’ ‘shida na Marijani Shabani’ zilikuwa mdomoni mwake kila dakika kufuatia mipigo redioni. Ilikuwa kazi ngumu kumshawishi mara chache aniruhusu kusikiliza taarifa za habari na vipindi vingine makini zaidi.

Ni kwa kupitia redio yake hiyo nilipofahamu kuwa Zanzibar, nchi ambayo ilitawaliwa na waarabu kwa muda mrefu, nayo ilikuwa ikiwaka moto kwa vuguvugu la kudai kujitawala.




Chama kilichoitwa Afro Shiraz kilikuwa kimeanzishwa na kuwapa taabu kubwa watawala.

Aidha, nilibaini kuwa hesabu ya watu ilifanywa mwaka 1957chini Tanganyika ilionyesha kuwa tulikuwa 9,087,6000 kati ya hao 364,072 au asilimia 4 tu wakiishi mijini.

Mwaka wa 1958 zikasikika habari za Julius Nyerere kushtakiwa mahakamani kwa kuandika katika gazeti la TANU, sauti ya TANU. Habari ambazo magavana wawili wa wilaya walidai kuwa ziliwadhalilisha. Nyerere alishinda shitaka moja na kutiwa hatiani kwa shitaka la pili. Adhabu yake ilikuwa kifungo cha miaka sita jela au faini ya shilingi 3,000/= alilipa faini. Kama asingelipa uenda tungejumuika naye gerezani humo.

Tukio hilo lilikuwa kama chachu ya matukio tele ya kisiasa yaliyoendelea kutumbuiza maisha yetu gerezani humo. Zilisikika habari za TANU kuchachamaa katika kudai uhuru. Zikasikika habari za chama kipya, ANC, kilichoongozwa na Zuberi Mwinyishehe Mtemvu, pia kiliomba ridhaa ya wananchi kuongoza serikali. Hatimaye, ikaja ile siku ya siku, desemba 9, 1961 tulikesha tukisikiliza redio, sauti ya Dar es salaam iliyokuwa ikitangazwa na bwana mmoja, Hamza Kasongo, kusheherekea uhuru. Ilipotimia saa sita za usiku tulisikiliza taarifa za bendera ya malkia wa Uingereza ikishushwa na ile ya Tanganyika ikipandishwa, Julius Nyerere akiwa Waziri Mkuu wa kwanza.

Pilikapilika hizo hazikuwa Tanganyika pekee. Kenya na Uganda pia kulikuwa kukiwaka moto. Lakini tukio lililonigusa ni lile la visiwa vya Zanzibar, Unguja na Pemba. Huko nako kulikuwa na purukushani kali za kisiasa. Mtu mmoja aliyeitwa Abeid Aman Karume na chama chake cha Afro Shiraz alikuwa



akusuguana na vyama vya ZPPP na ZNP. Uchaguzi uliojaa hila ulifanyika na kutoa madaraka kwa vyama vile vilivyokuwa na ushawishi mkubwa wa Waarabu dhidi ya Afro Shiraz iliyoshindwa kwa asilimia 54.3 januari 12, 1964 visiwa hivyo vililipuka, Waarabu wakatimuliwa, Karume na chama chake wakachukua uongozi.

Aril 21, 1964, pamoja na kuwa mfungwa nililala nikiwa Mtanganyika, kesho yake nikaamka nikiwa Mtanzania. Hiyo ilifuatia Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambao uliambatana na kubuniwa kwa jina jipya la nchi.

Nikiwa mfungwa kutokana na tuhuma za kuharibu maliasili na urithi wa taifa masikio yangu hayakuwa wazi kwa habari za kisiasa pekee. Nilitegemea siku hiyo habari zote zilizohusiana na mazingira, misitu na viumbe wake, maziwa na vyote vilivyomo na hata hali ya hewa. Kila nilipofanikiwa kupata gazeti nilifurahi zaidi na kulisoma lote, ikiwa pamoja na mashairi na kujaribu kujaza mafumbo.

Kupitia gazeti moja zile jitihada zilizobuniwa mwaka 1954, za kupandikiza aina mpya ya samaki katika ziwa Nyanza, ambalo sasa liliitwa Victoria, lilikuwa limetiliwa mkazo zaidi mwaka 1960 na kwamba jaribio hilo lilianza kutoa matunda. Hata hivyo, kulikuwa na malalamiko mengi toka kwa wana mazingira mbalimbali duniani kuwa samaki hao ambao ni wakubwa zaidi walikuwa wakiwateketeza samaki wa asili kwa kuwala. Hali ambayo ilielezewa kuwa iliashiria kuwa aina zipatazo hamsini za samaki wa ziwa hilo zilikuwa hatarini kutoweka.

Kwa upande mwingine nilijifunza kuwa serikali ilikuwa imeongeza jitihada za kuwalinda wanyama, miti na misitu asilia. Pamoja na Serengeti maeneo kama Ngorongoro, Ziwa Manyara,




Tarangire, Mikumi, Rubondo, Udzungwa na mengineyo tayari yalisajiliwa kama hifadhi maalumu za taifa. Maeneo mengine yalikuwa pamoja na Selow, Kilimanjaro, Gombe, Mahele na Katavi.

Hali kadhalika, mapori na misitu kadhaa ilihifadhiwa kwa ajili ya urithi. Selow yenye ukubwa wa takriban kilomita za mraba 50,000 ikiwa na maana kuwa inazishinda nchi kama Switzerland au Denmark kwa ukubwa lilikuwa eneo mojawapo. Ikiwa haina mtu anayeishi huko wala shughuli zozote za kibinadamu zinazofanyika, Selow inakadiriwa kuwa na tembo wapatao 60,000, nyati 160,000, viboko 40,000 na simba 5000. Pamoja na wanyama wengine anuai Selow inakisiwa kuwa na aina 440 za ndege. Ziwa Tagalala mto Rufiji, miti ya miombo na migunga pamoja na misitu inayoambaa na mito ni baadhi ya vivutio vinavyotajwa katika hifadhi hiyo.

Mapori mengine yaliyoifadhiwa yalikuwa pamoja na Moyowosi, Bugiri, Rungwa, Maswa, Kisiwa cha Saa Nane, Mkomazi na Ugala. Pia Usangu, Mpanga, Rukwa, Swaga, Ikorongo ni miongoni mwa mapori hayo.

Huko Zanzibar pia jithada tele zilikuwa zikifanyika kulinda mazingira ya nchi kavu na bahari. Pomboo, viumbe wa majini ambao wataalam hawapendi kuwaita samaki kwa kuwa wananyonyesha watoto wao, walikuwa wakitafutiwa namna ya kuwalinda. Vifo vya mara kwa mara vya viumbe hao, ambao ni wahamajihamaji vilikuwa vikisumbua sana vichwa vya wana mazingira. Viumbe hao, ambao wanafundishwa kwa urahisi hasa pale wanapochupa toka majini kama golikipa anayedaka mpira wanaweza kuwa kivutio kikubwa cha watalii.


* * *?






Pamoja na ‘alama’, kama kweli nilikuwa nayo nyota yangu ya kupendwa na watu bado ilikuwa iking’ara, hali ambayo naamini ilichangia kufanya niweze kuyamudu maisha ya gerezani humo hadi mwisho wa kifungo. Wakati wenzangu wengi walipigwa kama ng’ombe, baadhi wakifa kwa kutiliwa maanani wanapougua, mimi hali ilikuwa tofauti. Nilipendwa na mkuu wa gereza. Nilipendwa na maafisa wake pia. Nadhani kale ka usomi kangu kalisaidia. Mara kwa mara nilipewa kazi ya ukarani, kujaza fomu, kurekodi matumizi au mahitaji, kuandaa taarifa za wafungwa wenzangu na kadhalika. Kazi hizo zilipokuwa finyu nilipewa udobi wa kunyoosha nguo za askari magereza. Mara nyingine nilipewa kazi ya kutunza bustani ya mkuu wa gereza ambazo ziliambatana na kudokolewa chakula cha binadamu toka jikoni mwake.


Sherehe za uhuru na zile zilizofuatana mara kwa mara ziliambatana na kuachiwa kwa baadhi ya wafungwa wenye makosa madogomadogo au ambao tarehe zao za kufunguliwa zilikaribia. Bahati hiyo mimi haikunipitia. Uzito wa kosa langu haukuruhusu kunijadili katika kundi hilo. Kama ungeruhusu naamini nisingekuwa na sababu ya kusubiri tarehe iliyobandikwa kifuani pangu.


Uhuru wenyewe ulianza kunitia mashaka kabla sijauonja. Tulitarajia uhuru ulikuwa mwisho wa kero zote za Mtanganyika, ambaye sasa aliitwa Mtanzania. Tulidhani uhuru ungekuwa mwanzo wa neema na faraja kubwa nchini. Haikuwa hivyo. Nyimbo za hali ngumu ya maisha toka huko uraiani zilitushangaza sana wafungwa. Tulishangaa zaidi pale kasi ya watuhumiwa waliokuwa wakiletwa gerezani ilipoongezeka badala ya kupungua, wengi wakiwa watu wenye makosa ya ovyoovyo yaliyoashiria jambo moja kubwa ‘njaa!’



huyu kampiga mke wake hadi kumwua kwa kupoteza shilingi mia! Yule kafungwa kwa kuiba kuku wa jirani. Na Yule? Yeye alitupa kitoto kichanga jalalani!

Kasi hiyo, ilifanya selo zifurike, tuanze kulala ‘mzungu wa nne’. Huyu aliweka kichwa huku yule kule. Chakula kiliongezeka ubaya, hata hewa katika selo ilibadilika na kuwa nzito kutokana na kutumiwa na watu wengi kuliko ilivyokusudiwa.

Nadhani ni hali hiyo iliyoibua tatizo jingine zito zaidi, ‘maradhi.’ Zamani kidogo ugonjwa mkubwa gerezani ulikuwa malaria. Mara yaliingia maradhi mapya ya kipindupindu. Ugonjwa hatari wa kuharisha ambao ulimchukua binadamu siku mbili tu kupoteza maisha.

Wafungwa wengi walipoteza maisha, kutwa watu sita au zaidi hadi ulipodhibitiwa kwa vidonge vya kufunga tumbo. Tuliambiwa ugonjwa huu hatari chanzo chake kilikuwa uchafu. Lakini kutokana na shida ya maji gerezani humo, naamin tuliobakia hai ilikuwa kwa kudra za Mwenyezi Mungu zaidi ya jitihada kujikinga.

Habari za kipindupindu humo nje ya gereza pia zilivuma sana. Dar es salaam, Dodoma, Singida na kwingineko kipindupindu kiliteketeza maisha ya watu kama watu wa kusini wanavyoshambulia ‘dagaa nchanga’ au Wahaya wanavyowaonea ‘nsenene’. Sikuelewa hata kidogo kila nilipofikiria hilo. Watanzania tuteketee kwa uchafu kwa ajili ya uhaba wa maji! Nchi ambayo imezungukwa na maji kila upande, ikajaliwa mito, maziwa, mabwawa na chemchemi tele! Kwa kweli sikuweza kuelewa.

Wakati bado natafakari hilo, likaja jingine la kutisha zaidi, UKIMWI. Ugonjwa ambao wataalamu walidai kuwa




ulitokana na wadudu wanaoitwa HIV ambao hushambulia chembechembe nyeupe ambazo ni kinga ya mwili wa binadamu na kumwacha wazi kwa ugonjwa wowote kumtia mweleka wa mwisho. Niliwaona baadhi ya wafungwa wenye UKIMWI. Wanatisha kuliko chochote kile ulichopata kukiona. Nywele zao zilinyonyoka, mwili kuota mapele huku tumbo likiwa halina uwezo wa kuhifadhi chochote kutokana na kuharisha. Kama kipindupindu kiliogopwa kwa kuua haraka UKIMWI uliogopwa zaidi kwa kuchelewesha sana kumwua mteja wake huku ukimpa kila aina ya mateso.

Wajuzi wa masuala ya tiba walitueleza kuwa njia kubwa zaidi ya maambukizi ya UKIMWI ni katika kujamiiana bila kutumia kinga. Jambo ambalo mtu yeyote angeweza kulielewa mara moja na kujiepusha nalo. Lakini taarifa ya tatizo hilo huko nje lilikuwa kubwa na la kutisha kupita kiasi. Haikupita siku mbili bila kumsikia mfungwa mmoja wapo akiangua kilio. Kisa? Kafiwa na mdogo wake, mtoto wake, mke wake au rafiki yake. Taarifa za wasichana kujiuza katika majumba ya starehe, akina baba wenye pesa kuwarubuni wanafunzi, kuzagaa kwa mabaa na sehemu za starehe mitaani na vishawishi tele vya anasa ziliendelea kutufikia gerezani humo kwa kiwango kilekile cha kukua kwa kasi ya UKIMWI. Hali iliyoashiria kitu kimoja tu, hali ngumu maisha. Kwa lugha nyepesi; njaa!

Wakati huo tarehe yangu ya kumaliza kifungo ilizidi kukaribia. Siyo siri kwamba nilianza kuyaogopa maisha ya huko uraiani zaidi ya gerezani. Kama mazingira ya gerezani humo yangeweza kuboreshwa kidogo tu siyo siri, ningefikiria suala la kubaki gerezani humo wa makini zaidi.


?

21

Ben R. Mtobwa












YA ISHIRINI NA MOJA?

Mfungwa Mikono Musoma



W

anahistoria wanatukumbusha kuwa adhabu ya kifungo, ambayo mimi na wenzangu gerezani humu tulikuwa tukiitumikia,

ilianzishwa huko Ulaya yapata miaka 300 iliyopita.

Awali ya hapo mhalifu, au mtuhumiwa aliyepatikana na hatia ama alinyongwa ama alitoswa baharini au kuachwa katika visiwa vya mbali visivyo na watu.

Hapa Afrika pia tulikuwa na adhabu zetu mbalimbali. Mhalifu alilazimishwa kutoa baadhi ya mali zake kama adhabu, kutengwa na jamii yake hata kufukuzwa kijijini. Wakati mwingine alitungiwa nyimbo za mafumbo ambazo ziliimbwa katika sherehe na hivyo kumdhalilisha sana mbele ya jamii. Hali hiyo ilipunguza sana tabia ya uhalifu.

Hivyo, wageni walipoingia na kutushawishi kufuata dini na tamaduni zao kwa upande mmoja, upande wa pili walitushurutisha kutii sheria na adhabu zao. Moja ya adhabu hizo ni hili la gereza. Unakamatwa na mtu anayeitwa polisi, unapelekwa kwa mtu anayeitwa hakimu, kufumba na kufumbua uko mikononi mwa bwana magereza; ukifanya kazi ambazo hulipwi na kupewa chakula ambacho hushibi.

Ni katika hali hiyo tuliposhangazwa siku moja alipoletwa?



huyu kampiga mke wake hadi kumwua kwa kupoteza shilingi mia! Yule kafungwa kwa kuiba kuku wa jirani. Na Yule? Yeye alitupa kitoto kichanga jalalani!

Kasi hiyo, ilifanya selo zifurike, tuanze kulala ‘mzungu wa nne’. Huyu aliweka kichwa huku yule kule. Chakula kiliongezeka ubaya, hata hewa katika selo ilibadilika na kuwa nzito kutokana na kutumiwa na watu wengi kuliko ilivyokusudiwa.

Nadhani ni hali hiyo iliyoibua tatizo jingine zito zaidi, ‘maradhi.’ Zamani kidogo ugonjwa mkubwa gerezani ulikuwa malaria. Mara yaliingia maradhi mapya ya kipindupindu. Ugonjwa hatari wa kuharisha ambao ulimchukua binadamu siku mbili tu kupoteza maisha.

Wafungwa wengi walipoteza maisha, kutwa watu sita au zaidi hadi ulipodhibitiwa kwa vidonge vya kufunga tumbo. Tuliambiwa ugonjwa huu hatari chanzo chake kilikuwa uchafu. Lakini kutokana na shida ya maji gerezani humo, naamin tuliobakia hai ilikuwa kwa kudra za Mwenyezi Mungu zaidi ya jitihada kujikinga.

Habari za kipindupindu humo nje ya gereza pia zilivuma sana. Dar es salaam, Dodoma, Singida na kwingineko kipindupindu kiliteketeza maisha ya watu kama watu wa kusini wanavyoshambulia ‘dagaa nchanga’ au Wahaya wanavyowaonea ‘nsenene’. Sikuelewa hata kidogo kila nilipofikiria hilo. Watanzania tuteketee kwa uchafu kwa ajili ya uhaba wa maji! Nchi ambayo imezungukwa na maji kila upande, ikajaliwa mito, maziwa, mabwawa na chemchemi tele! Kwa kweli sikuweza kuelewa.

Wakati bado natafakari hilo, likaja jingine la kutisha zaidi, UKIMWI. Ugonjwa ambao wataalamu walidai kuwa




ulitokana na wadudu wanaoitwa HIV ambao hushambulia chembechembe nyeupe ambazo ni kinga ya mwili wa binadamu na kumwacha wazi kwa ugonjwa wowote kumtia mweleka wa mwisho. Niliwaona baadhi ya wafungwa wenye UKIMWI. Wanatisha kuliko chochote kile ulichopata kukiona. Nywele zao zilinyonyoka, mwili kuota mapele huku tumbo likiwa halina uwezo wa kuhifadhi chochote kutokana na kuharisha. Kama kipindupindu kiliogopwa kwa kuua haraka UKIMWI uliogopwa zaidi kwa kuchelewesha sana kumwua mteja wake huku ukimpa kila aina ya mateso.

Wajuzi wa masuala ya tiba walitueleza kuwa njia kubwa zaidi ya maambukizi ya UKIMWI ni katika kujamiiana bila kutumia kinga. Jambo ambalo mtu yeyote angeweza kulielewa mara moja na kujiepusha nalo. Lakini taarifa ya tatizo hilo huko nje lilikuwa kubwa na la kutisha kupita kiasi. Haikupita siku mbili bila kumsikia mfungwa mmoja wapo akiangua kilio. Kisa? Kafiwa na mdogo wake, mtoto wake, mke wake au rafiki yake. Taarifa za wasichana kujiuza katika majumba ya starehe, akina baba wenye pesa kuwarubuni wanafunzi, kuzagaa kwa mabaa na sehemu za starehe mitaani na vishawishi tele vya anasa ziliendelea kutufikia gerezani humo kwa kiwango kilekile cha kukua kwa kasi ya UKIMWI. Hali iliyoashiria kitu kimoja tu, hali ngumu maisha. Kwa lugha nyepesi; njaa!

Wakati huo tarehe yangu ya kumaliza kifungo ilizidi kukaribia. Siyo siri kwamba nilianza kuyaogopa maisha ya huko uraiani zaidi ya gerezani. Kama mazingira ya gerezani humo yangeweza kuboreshwa kidogo tu siyo siri, ningefikiria suala la kubaki gerezani humo wa makini zaidi.


?

21

Ben R. Mtobwa












YA ISHIRINI NA MOJA?

Mfungwa Mikono Musoma



W

anahistoria wanatukumbusha kuwa adhabu ya kifungo, ambayo mimi na wenzangu gerezani humu tulikuwa tukiitumikia,

ilianzishwa huko Ulaya yapata miaka 300 iliyopita.

Awali ya hapo mhalifu, au mtuhumiwa aliyepatikana na hatia ama alinyongwa ama alitoswa baharini au kuachwa katika visiwa vya mbali visivyo na watu.

Hapa Afrika pia tulikuwa na adhabu zetu mbalimbali. Mhalifu alilazimishwa kutoa baadhi ya mali zake kama adhabu, kutengwa na jamii yake hata kufukuzwa kijijini. Wakati mwingine alitungiwa nyimbo za mafumbo ambazo ziliimbwa katika sherehe na hivyo kumdhalilisha sana mbele ya jamii. Hali hiyo ilipunguza sana tabia ya uhalifu.

Hivyo, wageni walipoingia na kutushawishi kufuata dini na tamaduni zao kwa upande mmoja, upande wa pili walitushurutisha kutii sheria na adhabu zao. Moja ya adhabu hizo ni hili la gereza. Unakamatwa na mtu anayeitwa polisi, unapelekwa kwa mtu anayeitwa hakimu, kufumba na kufumbua uko mikononi mwa bwana magereza; ukifanya kazi ambazo hulipwi na kupewa chakula ambacho hushibi.

Ni katika hali hiyo tuliposhangazwa siku moja alipoletwa?



Nikasema, “Itabidi tutafute muda tukae na kusimuliana masaibu yetu kwa kituo.”

“Kuna ubaya gani?” Butiku alijibu.


* * *?

Mkoa wa Mara unapakana na nchi ya Kenya kwa upande wa kaskazini. Mkoa huo ambao unachangia neema ya ziwa Victoria na mikoa ya Mwanza na Kagera, Mashariki umepakana na mkoa wa Serengeti. Mji wa Tarime, alikozaliwa Matayo Butiku, au ‘Umsolopogaas’ kama anavyopenda kujiita, uko mpakani na Kenya. Mji huu ni maarufu kwa pilikapilika nyingi kama ilivyo miji mingine ya mipakani kama Namanga, na Tunduma uko katika wilaya ya Tarime, kando kidogo ya mpakani, Sirari.

Mkoa huo una sifa zote ambazo nchi hii imejaliwa; mvua za kutosha, ziwa lililojaa samaki, ardhi iliyojaa rutuba na mbuga za wanyama kama Ikorongo, Nata na baba lao; Serengeti.

Mara una makabila mengi ya asili na wahamiaji. Ya asili ni Wakurya, Wazanaki, Wajita na Wajaluo ambao pia, kama Wamasai, wana mizizi yao nchini Kenya. Wahamiaji ni pamoja na wahindi, Wanyarwanda, Warundi, Wahangaza na wengineo. Pamoja na sifa tele za neema katika nchi yao, watu wa?

Mara, hasa Wakurya wamerithi maradhi ambayo hadi leo tiba yake haijapata kupatikana; Ubabe. Mauaji na vita vinavyoitwa vya kikabila, ambavyo kwa kweli ni vita baina ya koo ndani ya kabila moja, vimekuwa vikitawala macho na masikio kupitia katika vyombo vya habari. Vijiji, kama Kubitarere, ni miongoni mwa vile ambavyo vimeathirika mara kwa mara na ubabe wa baadhi ya wanajamii wa ama Waachari ama Walyanchoka.




Kisa? Ama hawa wameshukiwa kuiba ng’ombe wa hawa, ama wamevamia shamba la hawa. Vita vitazuka, watu wanapoteza maisha, mashamba yanachomwa, nyumba zinabomolewa na uharibifu mwingine tele usio na kifani. Mara nyingi serikali, kupitia vyombo vyake vya usalama pekee ambayo huingilia vita hivyo na kuituliza. Lakini si kwa muda mrefu.

Ni mirathi hiyo ya hatari ambayo ilimgharimu rafiki yangu Matayo Butiku mikono yake yote miwili na kumpa kilema cha maisha.

Ilikuwaje?

Zilikuwa zimepita siku mbili toka nilipomtia machoni kwa mara ya kwanza akiwa katika hali ile. Tulipata wasaa wa kuzungumza, mimi nikifyeka majani yeye, aliyepangiwa kufyeka pia akipita hapa na pale huku akimwaga gumzo na vichekesho ambavyo nilibaini baadaye kuwa vilimsaidia sana kupatiwa huduma mbalimbali, ikiwa pamoja na kulishwa chakula.

“Tulipoachana pale shuleni mimi niliendelea kwa miaka miwili kabla sijaacha masomo na kurudi nyumbani ambako nilijiunga na shughuli za uvuvi katika ziwa Victoria. Baadaye niliacha kuvua na kuanza biashara ya kupeleka samaki Nairobi na Kampala.

“Unajua sangara hawaishi kuliwa tu?” aliniuliza ghafla. Sikumwelewa. Akafafanua, “Siku hizi sangara ni mali katika kila kiungo chake. Ngozi yake siku hizi ni mali ghafi inayotengeneza pochi murua za akina mama matajiri. Mifupa yake ni malighafi kwa viwanda vya mbolea na madawa. Siku si nyingi hata ile harufu yake itageuzwa manukato ya aina yake. Sangara ni almasi za ziwani.

“Nilipata fedha nyingi sana. Kwa viwango vya pale kijijini






nilikuwa tajiri. Nikajenga nyumba safi na shamba kubwa la miwa. Toka hapo ndipo mambo yalianza kwenda mrama.” Alisita kidogo.


Nikaitumia fursa hiyo kutumbukiza swali, “Ulikuwa hujabahatika kuoa?”


“Nini? Kuoa?” aliuliza huku akiangua kicheko. “Toka niko darasa la nne, wakati tukilala wote pale bwenini, mimi tayari nilikuwa na mke,” alisema.


Nikapigwa na butwaa. “Ulikuawa na mke!” “Naam.”


“Ulioa lini?”


“Sikuoa, niliozeshwa na ukoo wangu. Nilikuwa mtoto pekee wa kiume katika familia yangu. Dada zangu walikuwa kumi na mmoja. Walianza kuolewa. Tulipata ng’ombe wengi sana lakini wazazi hawakuridhika. Walihitaji mjukuu ili awe mrithi wa mali hizo na awapatie watoto wa kiume.”


“Uliwapata?” “Watu gani?”


“Watoto wa kiume.”


Nikamwona Matayo, kwa mara ya kwanza, akipoteza tabasamu na kuonyesha dalili za masikitiko. Nusu dakika tu, mara alirudia sura yake ya kawaida na kunijibu akisema, “Kuoa ni khiari, kuzaa ni majaliwa. Leo hii nina wake watano, hata mmoja hajanipatia mtoto wa kiume!”


Wake watano! Hata hivyo, sikushangaa sana. Matayo alikuwa mtu wa vituko na miujiza siku zote, muujiza wa kwanza ulikuwa ule wa kujiunga na shule akiwa ametuzidi umri wote darasani. Mwujiza wa pili ukiwa ule wa kuja shule na silaha zake zote. Sasa huu wa kwamba wakati wote alikuwa na mke!




“Hilo linakushangaza?” aliuliza baada ya kuyasoma mawazo yangu. “Kwa hiyo, utashangaa zaidi nikikwambia kuwa hata wakati tuko shule, kila likizo niliingia kwenye vita na kuwashikisha adabu adui zetu?”

Muujiza mwingine!

“Nilipigana sana. Na nilipata sifa tele za ushujaa. Adui zetu waliniogopa kuliko simba kwa njinsi nilivyokuwa hodari wa kupanga mashambulizi na kukwepa mishale na mikuki yao. Kwa kweli, jina la yule mzee wa Kizulu lilinistahili sana. Hadi leo sina mikono bado wananiogopa sana na kila vita niko mstari wa mbele nikiongoza mapambano. Kama nisingekamatwa na kushitakiwa wangenikoma.

“Ilikuwaje?” “Nini?”

“Ilitokea nini Umsolopogaas akaishiwa ujanja na kukatwa mikono?” nilifafanua.

Akacheka. Kisha akasema, “ Naweza kusema ndege mjanja hunaswa na tundu bovu. Nilifanya kosa la kumdharau adui yangu. Mtoto mdogo sana, tena ambaye alikuwa hajapigana vita yoyote. Tulivamia kijiji chao, tukateka mifugo yote. Watu wazima wote walikimbia, mtoto huyu, wa miaka kumi na moja au mbili aliachwa nyuma akilia. Mkononi alikuwa na sime.

“Nilikatazama katoto kale. Ka kiume! Ningeweza kukaua, ningeweza kukavunja shingo. Lakini nikakahurumia. Kwangu mtoto wa kiume alikuwa lulu. Nikakaacha na kugeuka ili niondoke zangu. Mara waa! Mkono wangu wa kulia uliokuwa na sime ukaanguka chini. Maumivu makali yakanishika, lakini hayakunishinda hasira niliyoipata. Nikageuka kwa kasi. Waa! Nilikutana na pigo la pili ambalo lilidondosha mkono wangu




wa pili. Maumivu hayakuwa na kifani. Bila khiari nilianguka na kupoteza fahamu. Nilipozinduka nilijikuta niko hospitali, mikono yangu tayari imekuwa vibutu.

Na nilipopata nafuu nilishtakiwa kwa mauaji na uporaji na kupewa adhabu hii ninayoitumikia.

Ilikuwa taarifa ya kusikitisha sana. Nilimhurumia, sikuwa na uwezo wa kumsaidia. Nikaishia kumpa pole tena. Nadhani nilimhurumia. Lakini kutokana na vitendo vyake mwenyewe na msimamo wake hata baada ya kupoteza mikono nilishindwa kuamini kama kweli ninamhurumia au la.

“Haya na wewe niambie kulikoni hadi ukafika hapa,” alisema. “Si walisema ukijua kupokea ujue na kutoa? Ama ukiwa mroho usiwe mchoyo?” aliongeza.

Yangu yanaelezeka kweli? Nilijiuliza.



M

Kiguu n2a Njia








2

YA ISHIRINI NA MBILI?

Hadi?


fungwa hana kauli. Mfungwa hana hiari. Mara tu ukishahukumiwa wewe si wewe tena, ni mali ya mtu mwingine. Utafuata matakwa

na hiari yake hadi mwisho wa kifungo chako.

Kwa mtu aliyekuwa na kifungo kirefu kama mimi, mfumo huo wa kanuni za mfungwa uliniathiri mara kwa mara, ingawa wakati mwingine athari hizo zilikuwa faraja kwangu kwa namna moja au nyingine.

Moja ya faraja hizo ni pale nilipobahatika kuwemo katika kundi la wafungwa walioteuliwa kwenda Zanzibar kusaidia kazi ya kuvuna karafuu. Kwa mujibu wa mkuu wa gereza karafuu zilipamba sana na zilikuwa zikielekea kuharibika. Vijana wa jeshi la kujenga uchumi wa huko walikuwa tayari wamepelekwa lakini hawakukidhi mahitaji.

ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog