Search This Blog

Thursday 29 December 2022

MPANGO WA NJE NI PIGO BUTU LA KIFO - 3

   

Simulizi : Mpango Wa Nje   Ni Pigo Butu La Kifo

Sehemu Ya Tatu (3)


"Amsuni....Tally Man!" Aliita Malfrey.




"Naam Bosi?" Muitikio wa pamoja ukasikika kutokea kwa watu wale. Malfrey Kobra akasema.




"Jina lake la kificho ni Black Scorpion mnatakiwa mumfahamu hivyo, ni mtu pekee aliyesimama upande wangu kwa muda mrefu.....!" (jinamizi la kula sauti likapita). Kimya cha ufupi kikapita Malfrey Kobra akimeza mate na kuvuta hewa mpya. Akaendelea.




".....alikubali kuwa mshirika wangu akichunguza mienendo ya siri inayofanywa na wanausalama wa nchini Tanzania mara baada ya kuwateka wale madaktari bingwa wa magonjwa ya Saratani na namna ya kujua jinsi ya kuyatibu ama kudili nayo. Kama sikuwahi kuwaeleza hili ni kwamba kaka yangu au pacha wangu Maleley Kobra alipoingia nchini hapa kama muwekezaji, alikuja kukumbana na mambo ya ajabu sana yaliyofanyika hapa nchini kiasi cha kumsababishia kaka yangu shida kubwa iliyokuwa ikiwahitaji wataalamu wenye uwezo mkubwa kumsaidia tiba au hata kuipoa ili afike kilele cha balaa lile. Nilijaribu kutafuta matabibu mbalimbali kutoka nchi tofauti za Afrika mashariki na kati na Afrika mashariki. Mtajiuliza kwanini sikwenda mbali....? Mtajua sababu iliyonifanya nisifike mbali kutafuta tiba ya ndugu yangu. Niliweka wapelelezi kwenye nchi tatu za Afrika mashariki ikiwepo Kenya, Uganda na Tanzania. Majibu nilikuja kuyapata kwenye nchi mbili baada ya upelelezi wangu kufanikiwa. Majibu hayo yalitoka Tanzania na Kenya nikachambua kati ya Tanzania na Kenya ipi itafaa. Nikaona nchi pekee yenye ufuatiliaji mdogo ni Tanzania tofauti na Kenya ambako sikuwa na msukumo nako sana. Nikafanya mpango wa kuwatorosha madaktari hao huku nikitumia jina la siri kwenye mpango huo ambao ulikuja kuwaficha madaktari hao.....!" Alimaliza kueleza Malfrey Kobra kisha akatulizana. Baada ya kutulia kwa muda huo mfupi akaendelea.




"......mtu huyu alikuwa ni miongoni mwa wanausalama wakorofi sana kwenye kitengo cha upelelezi ambacho kiliteua vijana wanne, mtu huyu kipindi hicho alikuwa na miaka 26 na alikuwa hana muda mrefu tangu atoke masomono hivyo kazi ya kumuingiza upande wangu ikawa ni nyepesi tu, pamoja na umri wake na ugeni wake kazini hata hivyo alikuwa ni mwiba mkali sana uliokuwa ukiogopesha harakati zetu na kuleta hofu kwenye maisha ya kaka yangu. Nikatafuta namna ya kumfanya awe chini yangu, nikatafuta namna ya kumfanya awe anachunguza upande ule na kuleta upande huu akakubali kwa kumlipa pesa nyingi zenye kubadili maisha yake kwa haraka na tukafikia muafaka kisha kuingia makubaliano ya kumlipa pesa nyingi kila baada ya mwezi. Akawa huku na sasa ni miaka kama ishirini imepita yuko huku hata hivyo hakuna mtu anayejua kwa kuwa anacheza pande zote kwa akili ya kuzaliwa." Akahitimisha Malfrey Kobra. Wale wawili wakamtazama Black Scorpion, Black Scorpion naye akawatazama kwa kuwageuzia shingo.


Wakatazamana.




"Kwanini yuko hapa Bosi na ilhali kazi ile ilishakwisha?" Akauliza Amsuni Bhehe. Malfrey akamtazama Amsuni kwa tabasamu pana.




"Iliwahi kwisha ndiyo hata hivyo kwa sasa imeibuliwa upya na Rais wa nchi hiyo, kama mnavyojua Rais wa sasa wa awamu hii anavyopenda sifa na alivyo mkali. Ameibuka na amri kali sana akidai kuwapata wataalamu wake wakiwa hai au wafu. Hii alinipenyezea huyu Black Scorpion mara baada ya mkuu wao wa usalama kutoka kwenye kikao kizito sana na chenye maazimio hayo ya kushtusha....! Si jambo dogo." Akaongea Malfrey. Amsuni Bhehe akaelewa baada ya kujibiwa.




"Black Scorpion!" Aliita Malfrey. Black Scorpion akaitika na kumtazama mgonjwa huyo.




"Nipe habari iliyoshiba sasa."




"Mkuu, mambo yanakwenda vizuri tangu kuingia kwangu hapa hata hivyo najua wajua kuwa mimi huwa siingii sehemu bila kuwa na sababu za msingi. Niingiapo mahali jua kuwa ipo sababu kubwa iliyoniingiza mahali hapo, ulinipa kazi ya kuhakikisha naondoa usumbufu wowote utakaojitokeza kwenye njia yako nikiwa nyumbani nchini Tanzania nami hilo ndilo nililolifanya kulingana na maelekezo yako. Nimefanya hivyo nchini Tanzania hata hivyo hapa nchini nimeingia na wanausalama na kwa tetesi tu nilizonazo hata jasusi hatari nchini humo pia yuko hapa...!"




"Yupi huyo?" Akauliza kwa hamaki Malfrey Kobra, loh!




"Sina hakika ni yupi kwa kuwa sijapata kumtia machoni hata hivyo ninayakini yupo."




"Umejuaje kama yupo?" Akauliza zaidi Malfrey Kobra.




"Wakati wa uteuzi wa wanausalama na walipokabidhiwa kazi hawakuwa wakipita sehemu ambayo haijapitwa na huyo jasusi, kilichopelekea mimi kujua ni namna mtu huyo anavyopita na namna anavyojua kuchunguza. Wanausalama walipoling'amua hilo ndipo nilipoweka umakini na kufanya upelelezi wangu nyuma ya ncha ya vichwa vyao hivyo kuwapa ugumu kunigundua kama nafuatilia nyendo zao. Wanausalama wako hapa hata hivyo jasusi hatari wa taifa la Tanzania yuko hapa pia amini hivyo bosi.....!"




"Black Scorpion, kama umejua wanausalama wako hapa je, umejua pia nini kilichowaleta? Maana ni miaka 20 sasa nikipiga hesabu zangu tangu kuwateka wataalamu wao?" Akauliza Malfrey akiwa ameanza kutokuelewa muenendo wa kazi yake jinsi atakavyoipeleka kama kuna vizingiti tayari. Black Scorpion akajibu.




"Kama nilivyowahi kutangulia kusema hapo awali ya kwamba, Rais ameamuru ipatikane hata mifupa yao na atakuwa radhi na mwenye kuridhia kuliko akiwa anashuhudia wataalamu wake wakipotea kabisa."


Aama!




Malfrey aliona ugumu wa kazi machoni mwake akajua fika hatakuwa akipambana na watu wachache bali atakuwa akipambana na watu wengi huku wengine wakiwa wabishi kwenye mpango huu hadi washuhudie ushindi. Alihitaji huduma aliyokuwa akiipata kutoka kwa Dokta mmoja aliyesalia baada ya mwingine kutokuwapo....!


Kutokuwapo...? Amekwenda wapi sasa...? Balaa.




Malfrey hakutaka kuona anamkosa daktari aliye naye hata kidogo kwani afya yake ilikuwa hatarini sana na mtu pekee wa kumsaidia ni tabibu aliyepo. Kama asipopata huduma ya daktari huyo ya mara kwa mara ni wazi naye anakabiliwa na kifo kama ilivyo kwa kaka yake Maleley Kobra. Akifa je, ni nani wa kuendeleza kisasi? Hakuna wa kuendeleza kisasi hivyo kulikuwa hakuna budi zaidi ya kupambana kufa na kupona hadi afikie lengo.




__________




Madaktari waliyotekwa kutoka Tanzania walikuwapo wawili, Dokta Omary Maboli Siki na Dokta Lumoso Papi Mmbai. Kwanini Malfrey ananadi kuwa anaihitaji huduma ya daktari aliyepo je, mwengine yuko wapi na aliyepo ni nani kati ya wawili hao? Hii ilikuwa ni michanganyano au mvurugano mkubwa sana wenyekuacha taharuki. Malfrey alimtazama Black Scorpion kwa nukta kadhaa kisha akarudisha macho yake mbele akivuta kumbukumbu fulani kabla ya kuongea chochote, utulivu wake ulipokuja kuvunjika akanyanyua tena macho kumtazama Black Scorpion.




"Usiku wa leo yaani ikiwezekana ukitoka hapa matekelezo yanafanyika kwa uwezo mkubwa na si tu yafanyike kwa uwezo mkubwa halafu iwe ndiyo imetoka mh, mh....! Si hivyo, yawe na ukamilifu usiokuwa na mashaka ndani yake." Aliweka utulivu tena kisha akanyanyua shingo kumtazama Amsuni Bhehe.




"Mpatie utambulisho wa Kiago Mathias." Akaagiza. Amsuni Bhehe akanyanyuka na kusonga hadi kwenye rafu moja ya vitabu pale sebuleni akavuta droo moja kutoka chini kabisa ya ile rafu na kutoa picha kadhaa kati ya hizo akateua moja na nyingine kuzirudisha mulemule ile moja akarudi nayo kikaoni. Akamkabidhi picha ike Black Scorpion kisha akasema.




"Kama ambavyo jina lake linasomeka nyuma ya hiyo picha kipande, anaishi kwenye mji wa Keno uliopo pembezoni kidogo mwa mji wa Ashura, nyumba namba (16). Ni mji mdogo hata hivyo tulivu sana kama ulivyo mji wa Ashura wenyewe. Mji huo wanaishi viongozi wengi sana hivyo pamoja na kuitwa Keno lakini pia umepachikwa jina jingine na kuitwa mji wa vigogo. Ni maarufu kwa jina hilo. Ukitoka Ashura hatua ishirini na tano mara baada ya kukivuka kibao kinachoitambulisha Keno.






Mji huo wanaishi viongozi wengi sana hivyo pamoja na kuitwa Keno lakini pia umepachikwa jina jingine na kuitwa mji wa vigogo. Ni maarufu kwa jina hilo. Ukitoka Ashura hatua ishirini na tano mara baada ya kukivuka kibao kinachoitambulisha Keno. Upande wa kushoto ndipo utakutana na nyumba hiyo." Akamaliza kutoa maelekezo Amsuni na kumtazama kijana huyo.




"Anatakiwa afe usiku huu na taarifa za kifo chake nizipate asubuhi kwenye vyombo vya habari." Alidakia Malfrey kisha akaweka utulivu. Mtu yule akajiondosha pasipo kusikiliza maagizo mengine. Malfrey akaondoshwa hapo pia hadi nje ambako kulikuwa na usafiri wa Chopa ndogo iliyokuwa ikimsubiri.




__________




Keno ilikuwa tulivu kwa majira hayo ya usiku na utulivu wake huu haukuwa kwa siku hiyo tu pekee bali ni utulivu endelevu wa mji huu kasia la upepo tulivu lilizidi kuchapa kwapa taratibu na kuifanya hali ya hewa ya mji huo kuendelea kuwa bora kuliko. Mbele ya lango la jumba kubwa lenye namba (16) kwa umbali mita zipatazo sabiini kutoka lango la jumba hilo lilipo, kulikuwa na pikipiki moja Boxer ikiwa imeegeshwa chini ya mti mmoja wa maua uliotanda matawi yake hadi chini na kufanya kuwe na kivuli cha giza nyakati hizo za usiku. Kivuli hicho kiliweza kuzifanya taa zilizokuwa zikifanya kazi kubwa ya kumulika eneo hilo la mbele, zisifanikiwe kuiona pikipiki hiyo. Kulikuwa na walinzi wawili kutoka kwenye jeshi la polisi ambao walikuwa wakizunguuka kwa kupeana zamu kisha baada ya mizunguuko yao ya kidoria kukamilika, walikutana kwenye kibanda kidogo cha ulinzi kilichopo pembeni ya lile lango. Huwezi amini kama eneo hili lilikwisha kuvamiwa na mvamiaji alikuwa akiusoma mchezo wote kuanzi anaingia eneo hilo hadi muda huo. Black Scorpion hakuwa mtu mdogo kwenye masuala haya ya kuuwa alijua mbinu zote za kuuwa na alijua kuzitumia. Alikuwa na ratiba yote ya jumba hili kuanzia ulinzi wake wa siri yaani wa CCTV kamera hadi walinzi wa dhahiri. Alifahamu kuwa nje kulikuwa na walinzi wawili ambao walijua vizuri kuzitumia silaha vizuri halafu ndani ya lango kulikuwa na mlinzi mmoja, huyu alikuwa na mafunzo ya mgambo tu hata hivyo wote walikuwa na silaha za moto na walijua kuzitumia. Katika kupeleleza kwake Black Scorpion kuhusiana na ulinzi wa CCTV kamera kama yupo mtu awaye macho masaa ishirini na nne kuziangalia, hakupata jibu la ndiyo, jibu alilolipata ni jibu la kwamba mtu pekee anayezifuatilia kamera hizo za ulinzi alikuwa ni muhusika mwenyewe wa nyumba hiyo na mara nyingi huangalia mgeni gani amemtembelea na kwa minajili ipi vilevile kwa wakati gani? Kinyume na hapo hakuwa na maana nyingine. Hii ikampa ushindi wa kwanza Black Scorpion. Uchunguzi wake wa pili ni kuhusu familia, alitaka kujua kama mzee huyu alikuwa akiishi na familia ndani ya jumba hilo. Hapa akapata kujua kuwa mzee huyu ni kweli alikuwa na familia ya mke mmoja na watoto wane wote wakiwa wakubwa na shughulizi zao hata hivyo mzee huyu amekuwa ni mtu wa kusafiri mara kwa mara mwishoni mwa mwezi kwenda Haika kwa ajili ya kwenda kuizuru familia yake. Aliishi mwenyewe na wafariji pekee walikuwa ni walinzi wake. Wakati anafika hapo kwenye hili jumba Black Scorpion palikuwa hapajafika hata mlinzi mmoja wa nje kwani kwa ratiba iliyopo ni kwamba vijana wanaolinda nje walikuwa wakifika hapo majira ya saa tatu usiku. Alifika hapo nyuma kidogo ya muda mara baada ya kupokea agizo. Aliweza kuwaona vijana wa jeshi la polisi ambao ndio waliotakiwa kuimarisha ulinzi wakati wanaingia na kufanya doria yao yeye akiwa kwenye jengo moja refu kidogo la ghorofa kama tatu hivi huku pikipiki aliyofika nayo hapo ikiwa imefichwa na yale matawi ya mti wa maua yaliyofungamana na kwa kuwa jengo alilopo halikuwa mbali na hapo wala hakutumia kioni chochote chenye kumpa msaada wa kuona mbali. Ni muda huu sasa alipopata wazo la kutoka kule alipo na kuifuata pikipiki yake wakati walinzi wale wakiwa wamejifungia kwenye kibanda chao cha ulinzi. Alipoifikia aliichukua kwa siri na kutoka nayo. Sasa pikipiki yake alifanikiwa kuiweka mbali kabisa na eneo lile, aliitelekeza pembeni ya duka moja la vyakula 'mini super market'. Uchunguzi wake ulivyokamilika ndipo alitoka alipo na kusogea kwa tahadhari kubwa hadi chini ya mti huo wa maua ikiwa tayari inakaribia saa sita na dakika zake nyingi tu. Alifika hapo baada ya kuona askari wale hawatoki baada kujiingiza kwenye kile kibanda chao ambacho kilikuwa na kioo kidogo ambacho kama mtu aliyeko ndani ya kibanda hicho akihitaji kuchungulia basi ni lazima aujaze upande wake wa jicho moja ndiyo atazame. Hata hapo alipofika pia hakufanya papara, alitulizana kimya kama maji yatuamavyo ndani ya Koa. Utulivu huu ukamfanya aweze kuzihesabu zile kamera zote kwa umakini mkubwa. Taa zilikuwa zikiwaka kwa ukali sana hivyo akajua kila kulipo na taa moja basi kuna kamera moja na uwezo wa kamera kufanya kazi hutegemea ukali wa taa husika nyakati hizo za usiku. Alishatosheka na upelelezi wake Black Scorpion na kwa wakati huo alikuwa akienda kutekeleza kazi na si kitu kingine. Jumba hili licha ya kuwa na walinzi hao hata hivyo lilikuwa na ulinzi wa sistim ya umeme, nyaya kadhaa zilipita juu ya ukuta mrefu wa uzio wa jengo hilo. Akiwa pale akiwa anazihesabu dakika zinavyoenda, kuna kitu kingine alikisikia hiki akaona kingeweza kumsaidia kwenye kazi yake, zile nyaya za umeme kwa kuwa zilikuwa zikipitisha umeme hivyo kulikuwako na sauti fulani ya mvumo ambayo ilikuwa ikivuma kila baada ya sekunde kumi na tano. Hili aliliweka akilini na sasa alikuwa amekamata kokoto ndogo nzito mkononi mwake huku mkono mwengine wa kuume ukiwa umekamata bastola aina ya Glock 35 iliyovikwa kiwambo cha kuzuia sauti. Hakuwa mbali na kibanda kile hivyo hakuwa na mashaka kuwa anaweza kufanya yaliyo mema kwa wakati husika. Alikuwa makini katika kuzihesabu sekunde, ilipofika sekunde ya kumi akairusha ile kokoto kwenye lango la kuingilia ndani ya uzio ule, sekunde ya kumi na nne kabla ya ule mvumo kutokea, jicho lake na shabaha yake ikahamia kwenye kile kioo cha kwenye kile kibanda. Mvumo wakati unaanza sekunde ya kumi na tano, ulianza mtoko wa risasi iliyokoholewa kwa kikohozi cha wastani kilichotoka kwenye bastola ya Glock 35 iliyovishwa kiwambo cha kuzuia sauti. Mguno mdogo ukasikika akajua nini kimetokea. kitendo kile alichokifanya kilikuwa cha kipekee sana. Alipotupa ile kokoto nzito langoni alijua fika mlinzi wa ndani angeweza kusikia kama angekuwa makini hata hivyo walinzi waliyoko kwenye kile kibanda wangetaka kujua ni nini kilisababisha sauti hiyo ya kupigwa kwa lango hivyo ni lazima mmoja kati ya wale wa ndani angechungulia kwenye kile kioo. Mbinu za kivita alizijua Black Scorpion, hivyo kwa shambulio hilo alikuwa na yakini kabisa kuwa aliyepo ndani yaani aliyesalia kabla ya kupata uhai wa kutoa taarifa mahali na kuomba msaada kwanza ni kuchachawa. Hakuwa na shaka na kugundulika na askari aliyeko ndani ya uzio kwani alitumia uwezo mkubwa sana wa kufikiri kabla ya kufanya maamuzi.




Alijirusha mithili ya nyani arukiyae tawi la mti au goli kipa anayeurukia mpira wa adhabu. Loh! Kwa haraka sana alijiviringisha mfano wa gogo litokalo mlimani baada ya kutemwa na wapasua mbao kutoka shinani mwa mtiwe, akaja kusimama kwenye ukuta mdogo wa kile kibanda cha ulinzi. Zilikuwa ni sekunde pekee ndizo zilizotumika. Hapa akasikia mhemo wa mtu aliyesalia ndani na kupaparuka kwake kwa hofu, alisikia kupitia kile kioo ambacho si kioo tena mara baada ya risasi kutoka kwake kufanya yake. Akajizungusha kuufuata ule ukuta hadi mahali palipo na kimlango kidogo ambacho kilikuwa wazi huku kichwa kilichokuwa kikivuja damu kikiwa kimelalia nje, akajua risasi yake ndiyo iliyofanya ya kweli. Akaitazama Glock 35. Bastola matata iliyobuniwa huko Austria mnamo mwaka 1990. Akaibusu kidogo pembeni ya kasiba yake. Akiwa hapo alisikia sauti ya simu mithili ya mtu aandikaye namba au achezeaye simu. Kwa uwezo na utaalamu wa kazi ya kijasusi akajua nini kilikuwa kikifanyika. Akanyata kidogo hadi ulipo mlango akaitanguliza kasiba ndani na kuvuta kilimi risasi mbili zikatoka, mvurugano ukasikika humo ndani na yowe dogo la maumivu kabla ya mtu huyo kutulia. Kazi ilishakwisha ya nje sasa ilibakia ya ndani. Ndani kuingia haikuwa kazi rahisi, ilihitaji utulivu wa akili na mwili hata hivyo hakuwa na muda mrefu wa kufikiri kwani ukaaji wake pale wa muda mrefu kilikuwa ni kielelezo tosha cha kuyajua mazingira ya eneo hilo. Akausogelea mlango huku akiitazama kamera ambayo aliamini pamoja na kamera hizo kumuona bado alikuwa na nafasi kubwa ya kuwa sirini kwa namna alivyo vaa. Akagonga mlango mdogo mara tatu kisha akatulia, akagonga tena mara tatu akatulia tena, safari hii alisikia mburuzano wa hatua ukiwa unajongea alipo akaikamatia silaha yake vema. Mlinzi wa ndani hakuwa na shaka kwa kuwa alijua fika ni askari wale ambao mara chache wamekuwa wakiingia ndani kuuliza hali ya usalama wa mzee kama ilivyo taratibu zao. Hivyo alivyofika hakuuliza alifungua mlango mdogo na kuchungulia nje, akastaajabu! Domo la bunduki likamtazama na mshika bunduki akamuomba awe mpole na walekee ndani.


Alipatikana kipumbavu tu.




"Wewe ni nani?" Akauliza mlinzi akiwa na hofu moyoni mwake.




"Mmoja wa walinzi wa jengo hili, hukuwahi kuniona?" Akajibu Black Scorpion.




"Hapana sijawahi kukuona!" Akasema mlinzi sura yake ikiwa imejaa tashwishi kubwa sana.




"Ooh! Sina muda mrefu tangu nihamishiwe kwenye lindo hili...mimi ni mgeni hapa na ninashida na Jaji, ni chumba kipi anachokitumia sitaki kupata shida katika kumtafuta." Akaongea Black Scorpion kisha akaitoa usalama bastola yake na kuihamisha toka kifuani hadi kwenye paji la uso la mlinzi huyo. Mlinzi yule akachachawa alijua nini maana ya silaha ikishatolewa usalama, mafunzo ya muda mrefu ya mgambo yalimsadia sana kujua tabia za silaha chache kwa uchache pia.




"Ni humu ndani....!"




"Najua ni humu ndani ila nataka kujua chumba anachokitumia kwa ajili ya kulala,"




"Si ndiyo nakuelekeza sasa aaah....! Shusha basi kidogo hiyo bastola chini....ni humu ndani, ukishaingia sebuleni chumba cha kwanza cha pili upande wa kushoto hicho ndicho chumba chake....usiniue tafadhali nina familia inani....!" Hakusubiriwa amalizie, ile kanuni ya ukitaka kumuua nyani ndiyo iliyotumika. Risasi moja iliyokifumua kichwa cha mlinzi yule ikampeleka chini kama mzigo huku akiwa hana alijualo. Hatua ndefu zikamfikisha mlangoni. Akatia ufunguo wake wa bandia kutoka kwenye mlundikano wa funguo nyingi atembeazo nazo hiyo ikiwa ni baada ya kuusukuma mlango ule na kuukuta ukiwa umefungwa. Mlango ule haukuleta kujua, ukafunguka taratibu. Kitu ambacho hakukijua ni yule askari aliyempiga risasi akiwa ndani ya kibanda. Alipoteza fahamu mara baada ya risasi zile mbili kumuingia mwilini moja ikiwa imepenya kwenye mbavu zake na kumpapuza nyama za ubavu na nyingine ikiwa imepiga kwenye paja. Punde alirudiwa na fahamu zake hata hivyo baada ya kuvuta kumbukumbu akaikumbuka hali ya mtu aliyekuwa anamlinda, akakumbuka kuwa alikuwa kibaruani pia akakumbuka jambo la hatari lilitokea hapo punde na kumuacha akiwa na majeraha. Akakamata silaha yake na kuzama ndani ya uzio akiwa anachechemea alipofika kwenye uzio ndani akamkuta mlinzi wa ndani akiwa hatamaniki kwa kumtazama, alipoangalia mlango wa kuingilia ndani. Nguvu zikawa zikitaka kumpotea tena hata hivyo alifanikiwa kujikaza na kulenga kivuli ambacho alikiona kikipotelea ndani na kuachia risasi zisizo na shabaha. Milipuko mitatu ya risasi ikasikika na kuleta hali ya wasiwasi kwa Jaji Kiago Mathias ambaye alikuwa akijiandaa kujilaza usiku huo kutokana na muda kwenda sana na uchovu wa mihangaiko yake ya kila siku. Jaji Kiago akatoka pale kitandani na kukimbilia kwenye kona moja ambako kulikuwa na tarakilishi moja ambayo iliunganishwa na kamera za ulinzi. Akarudisha matukio nyuma mara baada ya kuiwasha. Mh! Akagumia kwa ndani baada ya kuona kiumbe asichokitarajia kikifanya mambo ya ajabu kwa walinzi wake. Akakimbilia simu na kuipiga mahali, kikubwa alichokiongea ni kwamba amevamiwa na alihitaji msaada wa haraka mno. Alipomaliza kuongea hivyo akaishika bastola yake ndogo na fupi sana aina ya 2MM Kalibri kisha akatoka mule chumbani. Wakati anatoka, Black Scorpion alikuwa akicheza na akili ya mlio wa hiyo silaha akilini mwake akagundua kuwa mlipuko huo ni wa bunduki aina ya SMG. Moja kwa moja akahamisha mawazo yake kwa wale akari au huwenda kuna walinzi wengine hakuwa amewaona. Risasi zilimkosa kwa hatua chache tu hii ilikuwa na maana kuwa mpigaji hakuwa kwenye shabaha nzuri. Akarudi nyuma kwa tahadhari akafanikiwa kumuona mpigaji akiwa anasogea akiufuata mlango bila tahadhari huku akiwa anachechemea.










Moja kwa moja akahamisha mawazo yake kwa wale akari au huwenda kuna walinzi wengine hakuwa amewaona. Risasi zilimkosa kwa hatua chache tu hii ilikuwa na maana kuwa mpigaji hakuwa kwenye shabaha nzuri. Akarudi nyuma kwa tahadhari akafanikiwa kumuona mpigaji akiwa anasogea akiufuata mlango bila tahadhari huku akiwa anachechemea. Akatabasamu baada ya kumuona ni askari aliyekwisha kumjeruhi. Akapiga risasi yake moja iliyojaa kifuani vema kabisa na kumpeleka yule askari chini mazima. Alipomshusha yule askari akageuka nyuma na kukutana na kitu asichokitarajia, mzee akiwa tayari amemnyooshea mtutu wa bunduki.


Balaa!




Akajua dhahma hiyo, akajirusha kando na kubingiria kwenye sofa moja la hapo sebuleni akatambaa kwa kasi ya nyoka na kuibukia kwenye sofa jingine ambalo lilikuwa sambamba na Jaji Kiago Mathias. Kiago Mathias akapiga risasi iliyopiga hewa huku nyingine zikizama na kupotelea kwenye foronya laini ya sofa lile na muda huo huo Black Scorpion alijirusha na kumzawadia mzee huyo teke la kusukuma huku lile sofa akilitumia kama nyenzo iliyomuwezesha kujifyatua na kujirusha kama mshale. Mzee akajibabatiza kwenye Friji akajipigiza chini na kujigonga paji lake la uso mara baada ya kujipiga kwenye Friji na kutupwa chini. Hakujua bastola alipoiangushia. Damu zilikuwa zikimtoka puani na mdomoni kutokana na kule kujigonga vibaya sana nyuma ya kichwa chake pale kwenye lile Friji.




"Wewe...wewe ni nani na unataka nini kwangu?" Akauliza Kiago Mathias akijaribu kuiinua sura yake juu kwa sauti iliyopwaya.




"Mimi ni malaika wa mauti na nimekuja kuichukua roho yako!" Akajibu Black Scorpion kwa sauti iliyokuwa ikitafuta utulivu.




"Nani aliyekutum....!" Hakumalizia kuuliza, teke moja baya lililopigwa chini ya kidevu mara baada ya kuinyanyua sura yake juu, likambeba mzimamzima na kumtupa nyuma, damu zikamtoka kwa wingi huku akipaparika kama Mkizi aliyejirusha nchikavu mwa bahari. Alijing'ata vibaya sana ulimi wake kwa pigo lile mdomo ukalegea ukawa unatoa mate mazito ya damu pasipo kuyazuia.




"Unadhani malaika wa mauti anatumwa na nani? Anatumwa na shetani?....usidhani ulichokifanya miaka 16 iliyopita kilikuwa ni kitu cha kufurahisha. Ulisabisha watu kuikosa haki yao na wewe ukiwa ndiye mtoa hukumu ndani ya mahakama kuu. Adhabu uliyoitoa ni zaidi ya kifo cha maradhi kwa Maleley Kobra yaliyosababishwa nawe ambacho kilimuua mtu huyo. Hukujua kitu ulichokuwa ukikipanda, hukujua kwanini watu wanaishi kwenye mazingira magumu hadi sasa pasipo kufanya kazi yenye kuwaingizia mabilioni ya shilingi. Umeingiza hasara kubwa sana kwenye kampuni nyingi ukidhani unatenda haki...! Haki mbele ya maisha yako? Mpuuzi kweli wewe. Nakuuwa na hii ni ahadi ya malipizi kutoka kwa pacha wake Malfrey Kobra. Unajua ni kwanini nimekupa siri hii? Nimekupa hii siri kwa kuwa huwezi tena kwenda mahakamani na kutoa hukumu kwa Malfrey labda kama ukipewa ujaji mbinguni ndiyo utamuhukumu kwa mara ya pili Maleley Kobra, hataaa!.....hata ukifanya hivyo bado Malfrey atakuja kukuuwa tena." Akasema Black Scorpion kisha akampiga teke jingine la kifua, jingine na jingine, Kiago Mathias akatulia tuli damu zikikithiri eneo hilo.




__________




Huu ulikuwa ni mji tulivu sana hivyo hata ukiwa unatembe nyakati za usiku huwezi kupata wasiwasi. Nilishushwa mbali kidogo na nyumba niishio, nilifanya hivi makusudi ili nisiweze kujulikana ninapoishi. Niliisubiria teksi iliyonifikisha hapo iondoke ndipo nami nikapiga hatua zangu za taratibu kuelekea niishipo. Gari yangu nilikuwa nimeiacha kwenye nyumba niishio kwa makusudi kabisa kwani nilitaka nitembee muda mwingi kwa miguu ili niujue mji wa Ashura na vichochoro vyake kwa ujumla. Nilijifunza vingi nikiwa mjini hata hivyo sikuwa nimechoka sana japo nilitembea sana ndipo nikaonelea nichukue teksi moja mjini ambayo ilikuja kuniacha mahali hapo. Nilipoitazama saa yangu ya mkononi niligundua ilishatimia saa sita kasoro, usiku ulikuwa ukielekea kuwa mkubwa hata hivyo eneo nililopo halikuwa lenye kufikirisha sana na kukupa mashaka ya kuhofia muda. Nilikuwa napita pembezoni kabisa na kilipo kibao cha mji wa Keno, mji mtulivu zaidi ambao asilimia kubwa umejaa majengo ya viongozi, sehemu pekee iliyoutenganisha mji wa Ashura na Keno. Hofu yangu kubwa ilikuwa ni kukutana na askari tu wanaolinda maeneo hayo yaliyosheheni majengo mengi ya viongozi hata hivyo sikuwa na hofu nyingine ya kuhofia vibaka.




Usalama ulikuwepo wa kutosha wa askari japo sikutaka kukutana nao ili kuepuka maswali ya kukera. Nikiwa nazidi kuzirusha hatua zangu taratibu, mara nikasikia kishindo, kilikuwa ni kishindo kikubwa kilichopasua anga. Nikajiweka sawa ili kuipa akili utulivu na kwa uelewa wangu haraka sana nikagundua kuwa ilikuwa ni bunduki. Nikasita kutembea na kusikiliza kwa utulivu zaidi. Nikasikia tena na tena. Idadi ya milipuko ilifika mitatu kisha kimya.


Balaa!




Sikusuburi, nilitimua mbio kama niko kwenye Marathon, nilikimbia vibaya sana hadi nilipofika mahali ambapo nilihisi kuwa ndipo milipuko hiyo ya risasi ilipotokea. Nikatafuta kwenye kila jengo la hapo karibu kuona kama ningeona viashiria vya uwepo wa hatari iliyonivuta hadi kuwa hapo. Sikuona. Nikageuka nyuma kwenye jengo moja tulivu, nikalitazama kwa udadisi mkubwa huku nywele zikianza kunisimama mapigo ya moyo yakibadili upigaji. Nilipotazama kwa umakini zaidi, niliona kitu ambacho kilinivuta, nikasogea huku bastola yangu ikiwa imara mkononi. Alikuwa kama mtu aliyejibana kwenye kona moja ya ukuta wa uzio wa jengo hilo. Nikatambaa na ukuta nikikingwa na maua marefu, nikasogea zaidi huku mwili ukinichemka vibaya sana nilipokaribia na kutazama kwa ukaribu zaidi hata hivyo hakukuwa na kitu chenye kuleta mashaka, lilikuwa ni Ua kubwa lililopambwa na weusi wa giza huku likiwa limekatiwa kitaalamu sana na kuleta wasiwasi kwa upande wangu. Nikashusha pumzi nzito sana nikiuita utulivu ili niiweke akili yangu sawa. Nikageuka nyuma katika kujihakikishia usalama nako nikaona kimya tena eneo hilo halikuwa hata na ulinzi wa kutosha, nikakimbia tena kwenda mbele zaidi. Baada ya mwendo mfupi mbele, nikasimama ghafula baada ya kuona jengo moja likiwa katika hali isiyo sawa. Nje kulikuwa na kibanda cha ulinzi hata hivyo jicho langu lilifanikiwa kuona hali isiyo ya kawaida kwani niliona kioo kidogo kilichotumiwa na walio ndani kuona nje, kikiwa kimevunjwa. Akili ikaganda kwa sekunde kadhaa kabla ya kupata uhai tena. Nilisogea eneo hilo kwa tahadhari ya hali ya juu sana, nilipofika nikautafuta mlango ulipo na kuchungulia ndani yake. Kimya kilikuwa kikubwa na sikuona chochote zaidi ya mwili uliolala na kichwa chake kujaa mlangoni pale, nilipoangalia ndani vizuri, sikuona kitu kingine tena zaidi ya bunduki moja aiana ya SMG ikiwa imeulalia ule mwili usio na uhai upande wa miguuni. Hali hii iliniumiza sana na nilianza kuwa na wasiwasi mkubwa na usalama wangu.




Kuna watu wana roho mbaya sijapata kuona kwenye uhai wangu! Niliwaza. Nilikataa kabisa kama huyu au hawa waliyofanya hivi walikuwa ni wanadamu wa kawaida, nikairudisha bastola yangu kiunoni taratibu nikijaribu kuzunguusha macho yangu kila upande wa eneo hilo. Sikupoteza muda tena nilielekea ndani huku nikijiridhisha na uwepo wa silaha yangu kiunoni. Nilipoufungua ule mlango mdogo, niliona mwili wa mlinzi mwingine ukiwa umelala ndani ya ule uzio. Damu zikanichemka mwilini hali ya hatari ikijionesha wazi wazi. Nilijaribu kujiuliza kuhusu mtu aliyekuwa akiishi hapa kwenye jengo hili hata hivyo niliachana na maswali hayo kwani sikujua namna ya kuyapatia majibu. Niliusukuma mlango huku nikiitoa bastola yangu kiunoni na kuiweka mkononi barabara, mlango ule mdogo wa langoni ulipokuwa wazi kwa kiasi cha kuweza kuona ndani, nikasikia kukurukakara kwenye sebule ile huku kishindo kidogo cha kufungwa kwa mlango kwa nguvu kikisikika, nikachungulia huku bastola yangu ikitangulia. Nikageuka nyuma katika kuweka utahadhari, nikaona mwili wa mlinzi mwengine ukiwa unavuja damu sehemu mbalimbali za mwili wake na mwili huo ulikuwa ukifanana na ule wa yule askari aliyeko kule kwenye kibanda cha ulinzi nje kimavazi. Nikaachana na huo mwili nikiayarudisha macho yangu mbele huku akili yangu ikiwa makini zaidi. Mara nikasikia kwa mbali purukushani zikisika chumbani mithili ya mtu apapatuaye dirisha kutaka kujipatia upennyo. Akili yangu ikakataa kusonga mbele zaidi, nikarudi nyuma nikiwa kwenye tahadhari bado. Nikiwa pale mlangoni kurudi nilipotoka, kishindo kingine kidogo sana kilichohitaji utulivu kusikika nilikisikia kwa upande wa nje, sikupoteza muda nilitoka kabisa na kusimama kwenye uzio ule. Nilimuona mtu akiwa kwenye mavazi meusi tupu, mrefu mwenye mwili wa saizi ya kati akiwa anatokea upande wa nyuma kwenye kona. Nilijirusha chini kisha nikabingilia kama gurudumu la pikipiki lililosukumwa na mtoto, hisia zangu zilikuwa sahihi maana nilipotoka eneo nililokuwa nimesimama palipita risasi ambayo ilokusudia kunimaliza. Ilinikosa ikachimba ukuta hata hivyo alikuwa ni mwenye shabaha kali sana na kama ningezembea ningekutana nayo. Sikutulia sehemu moja nilibingilia huku nikirusha risasi kumchanganya mtu huyo na kumpotezea umakini na shabaha. Ilikuwa ni vigumu kumjua na yeye kunijua pia kwani kulikuwa na mwanga hafifu eneo lile na hali hiyo ilisababishwa naye kwa kuvunja taa mbili za eneo hilo la mbele alipokuwa akitupa zile risasi bila mpangilio. Nilisogea hadi kwenye maua fulani hapo nikatulia nikimtazama mtu yule mweusi. Nikamuona akisota chini kisha akasimama na kuanza kutimua mbio kwa mtindo wa ajabu sana wa zigi zaga akiwahi pale langoni.


Alitaka kunikimbia. Oouh!




Hakuwa mtu mdogo kwenye kujua kucheza na akili za adui. Sikuwa mbali na ulipo mlango wa kutokea nje ya uzio huo, nilikuwa karibu sana na kilichokuwa kimenifikisha hapo ni ule ujanja wa kubingilia kama ninja. Nilikuwa nikizitazama mbwembwe zake kwa ukaribu zaidi huku nikifikiria namna ya kufanya. Kama ningetaka kumuua ilikuwa rahisi sana. Maana mwili wake anavyourusha haikuwa sababu ya risasi yangu kumkosa, ila sikutaka kukurupuka, kwanza nilitaka kujua amuzi lake la mwisho ni nini. Akawa ameukaribia mlango, hapa sikusubiri, nilipiga risasi moja iliyomkosa kwa nafasi ndogo, hii nilikusudia kumkosa. Wakati anarudi nyuma kwa hofu, nilikuwa tayari nimeshajirusha hewani na kumvamia tukabingilia wote chini huku kila mmoja akiwa makini na silaha yake isiweze kumtoka mkononi. Tulibingilishana huku nikijitahidi kuitafuta nafasi ya kuweza kumuweka chini ili niweze kumuadhibu vizuri, alikuwa akicheza na akili yangu. Hakuruhusu nifanye nitakavyo, akanirushia ngumi kali iliyonikosa na kupita mbele ya pua yangu, nikamporomoshea tusi baya sana lililozidi kumpandisha hasira.




"Kumbe ni kahaba tu." Akabwata.




"Kahaba ni mama yako mzazi aliyejua kukuzaa na kushindwa kukulea!" Nilimrudishia maumivu. Nilikuwa nimemtusi tusi ambalo kwa mwanaume yeyote mwenye upendo na mama yake mzazi lazima angetokwa na povu. Nilifanikiwa. Alirusha ngumi nyingine mbili, moja nikaizuia na ya pili pia nikaipangulia mbali akaleta nyingine nikaizuia pia. Alipoona hafanikiwi akapiga ngumi moja nzito kwa hasira nikaizuia japo kwa shida kisha nikaikamata mikono yake vema na kuikusanya pamoja kifuani mwake huku bastoka zetu zikiwa mbali nasi.


Duu!




Huyu jamaa alikuwa fundi. Alinichapa kichwa cha mwamba wa pua hadi nikahisi kamasi nyembamba za moto zikinichoma puani. Mikono niliilegeza ikikosa nguvu ya kumzuia, hii ikawa nafasi kwake ya kunisukuma kwa guu lake na kunitoa pale juu. Akakurupuka kutaka kunitoka.


Nikakataa katakata.








Huyu jamaa alikuwa fundi. Alinichapa kichwa cha mwamba wa pua hadi nikahisi kamasi nyembamba za moto zikinichoma puani. Mikono niliilegeza ikikosa nguvu ya kumzuia, hii ikawa nafasi kwake ya kunisukuma kwa guu lake na kunitoa pale juu. Akakurupuka kutaka kunitoka.


Nikakataa katakata.




Niliudaka mguu wake mmoja. Akadondoka nikamrukia na ngumi ya sikio la kushoto akabweka kama Paka aliyekabwa na mwiba wa samaki kooni. Nikajizunguusha pale mgongoni na kumpiga ngumi nyingine ya sikio. Akalia tena hata hivyo akanipiga na teke la nyuma lililonitupa nyuma mbali naye, akadhani ameniweza akainyanyua sura yake ili kunivamia, nilikuwa nimeshageuka, teke moja kavu likapiga shavu lake la kushoto nikamgeuza chali. Akabingilia na kusimama akanikuta nikiwa wima tayari.




"Wewe ni nani?" Akaniuliza.




"Ninayezuia mauaji yasiendelee." Nilimjibu huku nikiwa tenge tayari.




"Kama nani?" Akaniuliza tena. Hatakakama sikuiona sura yake nilijua fika alikuwa yupo kwenye wasiwasi mkubwa.




"Operesheni Safisha!" Nilimjibu nikiwa makini kabisa na kumtazama, nilijua lazima achachawe kwa kumwambia hivyo kwani AKM alishanigusia mpango wa serikali yao ambao uko chini ya usalama wa taifa. Akashtuka wazi wazi na kunifuata kwa mtindo wa pekee sana hata hivyo akanikuta nikiwa imara, hakuambua kitu kwenye mapigo yake niliyazuia na kumpelekea ngumi moja safi ilimuingia kwenye kidevu akaja kama mbogo na kurusha ngumi kama tatu. Mbili nilizipisha moja ikatua kifuani maana alikuwa akizirusha huku akija mbele kama mwana Kipepeo. Mtindo huu ukampendezea akautumia zaidi nikajitahidi kuzuia ngumi nyingi hadi nilipoikamata mikono yake kisha nikamtandika kichwa kikali sana kilichotua juu ya jicho la kulia na kumpasua kidogo chini ya nyusi zake. Akapepesuka na kuuvamia mlango. Mlango kwa kuwa ulikuwa wazi akapotelea nje.




"Nitakutafuta siku nyingine nikimaliza kazi yangu." Akapayuka. Sikumfuata, nikageuka nyuma na kutazama chini kulikuwa na bastola mbili ya kwangu na ya kwake nikaziokota zote na kuzifutika kwenye maficho yangu. Nikazama ndani huku jazanda la yule mwanaharamu niliyepambana naye likijaa kichwani pasi na kutoka. Nilipofika sebuleni nikaukuta mwili wa mmiliki wa jengo hili ukiwa chini damu zikimalizikia kumtoka ilhali akiwa ameanza kuwa wa baridi. Baadhi ya sehemu damu ilishaganda tayari.




Kwa kuwa milipuko ya bunduki ilikuwa mikubwa hivyo niliamini askariwa watakuwa wamekwisha kuzipata taarifa tayari. Niliamini hivyo. Nikaikagua hii sebule kwa umakini mkubwa. Ilikuwa ni sebule ya kisasa yenye kila kitu kifaacho kuwapo hata hivyo kulikuwa na mapicha kadhaa ya urembo yaliyobandikwa ukutani ambayo yalibuniwa na fundi wa sanaa za mikono. Niliyagandisha macho yangu nilipoitazama picha moja ukutani, ilikuwa ni picha ya bwana huyo akiwa kwenye suti safi kabisa hata hivyo kulikuwa na picha nyingine hii alikuwa kwenye uvaaji wa kikazi zaidi.




Jaji. Nikawaza. Nikatazama kila mahali na kufika mahali ambako nilikutana na sehemu ambayo inaunganisha mfumo wote wa umeme mule ndani. Hadi sistimu ya ulinzi. Nikazima swichi kubwa giza likajaa, nikawasha kisha nikaelekea chumbani ambako nilikuta tarakilishi moja pembeni iliyotengwa nikaiwasha, nikiwa sijatazama chochote nikasikia kishindo kikubwa langoni. Nikakimbilia dirishani na kuvuta kioo pembeni nikachungulia.


Polisi!




Nilishtuka. Hawakuwa wachache walikuwa wengi mno. Nikastaajabu taarifa za kuja hapa walizipata wapi? Nilikuwa kama niliyechanganyikiwa kwa kuwa maswali niliyojiuliza yalikuwa yakipuuzi sana, kulikuwa na sababu kubwa za askari kufika hapo kikubwa hasa kikiwa ni ile milipuko ya bunduki. Nikarudi pale kwenye ile tarakilishi haraka sana kisha nikachomoa mkanda mzima uliyokuwa ukirekodi taarifa zote zilizopita kisha nikaelekea sebuleni kwa haraka kubwa kabla polisi hawajavamia ndani. Nikapita kwenye korido nyembamba ambayo ilinifikisha kwenye chumba ambacho kilihusika na umeme wote wa jengo hilo. Nikazima ile sehemu inayomiliki mfumo wa umeme wa nyumba nzima. Giza lile liliwashtua sana, mimi sikupoteza muda nilitafuta dirisha lolote la kunitoa upande wa nyuna. Nikapata moja ambapo nililifungua na kulitumia kujitoa ndani humo. Lile giza nilijua litakuwa kikwazo kwao nami niliitumia nafasi hiyohiyo kuparamia ukuta na kujipindua nje sikuwa na hofu ya umeme kwani nilizima kila kitu na muwashaji angechukua muda sana kung'amua jambo hilo. Nilitua upande wa nje kwa kishindo hafifu kisha nikapotelea gizani.




"Alikuwa nani yule mtu ambaye alijipanga kikazi zaidi kwani hata sura yake haikuwa ikionekana hata hivyo alikuwa na usafiri wa pikipiki kwani alipochoropoka mikononi mwangu na kukimbia nje, baada ya muda mfupi nilisikia muungurumo wa pikipiki ikitokomea?" Nilijiuliza hata hivyo sikuwa na jibu zuri. Sikumjua na nisingemjua kwa namna hiyo ya uulizaji wa kujiuliza mwenyewe. Nilikuwa sebuleni kwangu, nikiwaza yote hayo. Nilivuta tarakilishi na kuupachika ule mkanda na kuutazama taratibu. Mengi yalikuwa ni matukio ya kawaida. Wageni wa hapa na pale, wapita njia, na wengine waliopenda kupiga picha mbele ya jengo hilo, hawa walikuwa ni watu waishio nje ya mji huo. Nikiwa nazidi kuutazama ule mkanda, nikaona mtu aliye katika mavazi yale ambayo alivaa mtu niliyepambana naye. Nikaangalia muda ambao nilianza kumuona mtu huyo, nikafuatilia mwenendo wake hadi pale alipoamua kuanza kushambulia wale askari. Nikajua mtu huyu hakuwa mdogo kwenye masuala ya uuaji. Alitumia muda mrefu mno hadi kufikia maamuzi. Kwa muda alioutumia kwa mtu makini ni lazima awe amesoma kila kilichopo pale.


Huyu mtu ni nani? Nikawaza.




"Ni mwepesi na mwenye kutumia akili zaidi. Sikuweza kumng'amua mapema, katika uchunguzi wangu wa kichwani. Na pia ilikuwa ni vigumu kumjua kwa kuwa hata yeye alishajua kuwa eneo lile lina kamera.


Umeona balaa lilipo.


"Sikubali lazima nitamjua na atasema yeye ni nani na kwanini anaua?" Nilijisemea mwenyewe na huyu ndiye niliamua kumpa shutuma zote kwa sasa hadi pale nitakapopata na muhusika mwingine.




_________




Kwa kuwa polisi waliweza kupata taarifa usiku na kuwahi eneo la tukio, hii ikawa ni habari kubwa zaidi ambayo iliamka masikioni mwa watu wengi. Kila mja muungwana asubuhi alizipata taarifa za kifo cha Kiago Mathias. Taarifa hizi zilianza kuleta hofu kubwa sasa kwa vigogo wa ngazi za juu kabisa mwa taifa hili la Ungamo.


Kwanini Kiago?




Maswali ya mumo kwa humo yakaulizwa, jibu lilikuwepo japo wajibuji walichelewa kufika mahali palipoulizwa maswali. Labda wamsubiri. Ni nani sasa...?


Tafarani.




Taarifa hii ikaimeza taarifa nyingine ambayo ilitokea usiku huohuo na hii ilikuwa ni ya kifo cha aliyekuwa muendesha mashtaka wa mahakama ya Makutano. Masuka Mvungi. Kifo hiki hakikupewa umaarufu na raia mashuhuda kama kilivyo kifo cha aliyewahi kuwa jaji wa mahaka kuu. Taifa la Ungamo likaingia kwenye wasiwasi mkubwa sana kuhusiana na vifo vilivyokuwa vikiendelea. Upande mwingine ulikuwa na furaha baada ya tukio hilo kwani Malfrey alijiona ni mshindi kutokana na vijana wa Amsuni Bhehe, Abdi Hussein na Welasson kutenda vile ambavyo walitakiwa kutenda. Kifo cha Masuka wao ndiyo watekelezaji wake.




"Kwanini wapelelezi waliopewa kazi hawakufika kweye kifo hata kimoja na kumbaini adui ni nani?" Akauliza waziri wa ulinzi na usalama wa nchi akiwa mbele ya Domolangu Mabisu. Lilikuwa ni swali gumu sana kuweza kujibika mbaya zaidi waziri mwenye dhamana ya wizara hiyo ya ulinzi na usalama alikuwa ameyatoa macho yake fotoo! Akisubiri jibu. Domolangu Mabisu alikuna kidevu kwa sekunde kadhaa kisha;




"Vijana wako karibu na adui muheshimiwa na wako karibu sana." Akajibu.




"Wako karibu lakini hawana mpango wa kumkamata muuaji?" Akauliza tena.




"Hapana muheshimiwa,"




"Namjibu nini mkuu wa nchi akihitaji majibu kuhusiana na hili?" Jibu la swali hili lilikuwa gumu zaidi kiasi likampa mafikirio makubwa bwana Domolangu Mabisu. Hakusumbuka namna ya kujibu bali aliamua kujipa utulivu wa sekunde kadhaa ndipo akamtazama muheshimiwa huyo.




"Siku tatu jibu la kuridhisha la vitendo litakuwa mezani." Akajibu kwa kujiamini.




"Unauhakika?" Akahoji katika msisitizo.




"Kabisa." Akajibu akiwa amepata nguvu baada ya kuona ameanza kuachiwa nafasi ya kuvuta hewa mara baada ya kubanwa kwa maswali.




"Siku tatu zikipita hutakutana na mimi tena bali utajibu Ikulu majibu hayahaya kama unayonijibu mimi hapa." Akamaliza kuongea muheshimiwa Waziri kwa kitisho akasimama na kutoka ofisini humo huku jicho kali la Domolangu Mabisu likimtazama nyuma yake.




MAMBO YANAZIDI KUWA TETE HEE!








"Siku tatu zikipita hutakutana na mimi tena bali utajibu Ikulu majibu hayahaya kama unayonijibu mimi hapa." Akamaliza kuongea muheshimiwa Waziri kwa kitisho akasimama na kutoka ofisini humo huku jicho kali la Domolangu Mabisu likimtazama nyuma yake.




Hawa wapuuzi watasababisha kibarua changu kiwe mashakani? Akawaza Domolangu Mabisu. Akachomoa sigara moja kutoka kwenye mfuko wa shati na kuipachika kwenye kingo zake za mdomo na kwa msaada wa kiberiti cha gesi akaichoma. Moshi mwingi ukaimeza ofisi yake. Akaminya namba kadhaa kwenye kibweta cha simu ya mezani na kuweka kiwambo cha simu sikioni.




"Marietha, uko wapi kwa sasa?" Akauliza Domolangu Mabisu huku akiwa ameghadhibika mno.




"Tuko nyumbani kwa Masuka Mvungi ni punde tu tumetoka kwa Kiago Mathias...!"




"Nawaona mnavyozuru misiba yote kama wachimba makaburi, hivi mtakuwa wafuata matokeo ya matatizo hadi lini ninyi?" Akafoka Domolangu Mabisu huku sigara ikiwa mikononi mwake katikati ya pacha ya vidole vyake.




"Mkuu, mpigie kiongozi akupe maelekezo yaliyoshiba,"




"Halafu kuhusu kazi niliyokupa?" Akahoji tena Mabisu.




"Hiyo majibu yake ni ndani ya siku tatu bado nakusanya ushahidi wa kutosha," akajibu Marietha.




"Sawa hebu mpe simu Sembuyagi," akaagiza Mabisu. Simu ikapelekwa kwa Sembuyagi bwana huyo akaiweka sikioni.




"Ndiyo mkuu?" Akaitika.




"Niambie mahali mlipo hadi sasa?" Akahoji Mabisu.




"Hali inaridhisha nadhani tuko usoni mwa mafanikio tumejaribu kuchunguza na kuna kitu tumegundua kupitia haya mauaji yaliyojitokeza."




"Kitu gani mmegundua?" Akauliza zaidi.




"Mkuu, wacha tumalize kuchunguza hapa kwa Masuka kisha tutakupa majibu yaliyoshiba."




"Nasubiri muda huu!"




"Sawa mkuu!" Akaitikia kisha simu ikakatwa. Sembuyagi alikuwa yupo kwenye muonekano wa pekee sana ambao aliamua kutoka nao, huu ulikuwa ni wa tofauti kubwa na hakuwahi kuutumia muonekano huu tangu kuonekana kwake ndani ya jiji hilo la Muavengero. Alivaa kofia ya kapelo iliyotaka kuyafunika macho yake sambamba na miwani ya jua kubwa iliyoyafunika macho yake kwa kiasi kikubwa. Chini alivaa buti kubwa la jeshi kama kawaida na suruali ya jeans sambamba na fulana ya mikono mirefu ya rangi nyekundu. Miwani na kofia vilikuwa vitu vigeni sana kwa bwana huyo hii ilikuwa ni aina mpya ya uvaaji na mikato aliyotoka nayo siku hii ikamuweka tofauti zaidi. Waliingia ndani ya nyumba ya Masuka Mvungi iliyotawaliwa na vilio vya hapa na pale vya akina mama, nyumba ya Masuka Mvungi haikuwa kwenye eneo la watu wa hali ya juu bali lilikuwa kwenye maeneo ya kawaida hivyo hata ujaaji wa watu eneo la tukio ulikuwa ni mkubwa ukilinganisha na walipotoka nyumbani kwa Kiago Mathias ambako kulikuwa na watu wa kuhesabika. Hili la wingi wa watu halikuwazuia wanausalama hao kufanya kazi yao, kilichowapa ugumu ni polisi kwani nao walishafika mapema tu mara walipozipata taarifa za mauaji hayo yaliyotokea usiku pia. Walifika hadi barazani wakawakuta polisi wakiwa wameweka kizingiti cha kuzuia yeyote aliyetaka kuingia ndani kwa kile wasemacho kuwa walikuwa kwenye uchunguzi. Sembuyagi Mpauko Haufi aliyazungusha macho yake kwenye eneo lote lile na kugundua kuwa kuna askari mmoja ndiye aliyechukua jukumu la kuwahoji watu wa karibu wa marehemu angalau kupata chochote kwenye tukio hilo. Sembuyagi akasogea hadi karibu na askari yule ambaye kwa kumtazama tu kupitia alama za cheo alizobandikwa kwenye gwanda lake la kiaskari, ilionesha wazi alikuwa na cheo cha Koplo. Alikuwa na lengo la kutaka kupata kitu kutoka kwa askari hao ili kujua namna ya kuweza kupambana na jambo hilo ambalo lilishaanza kuwa gumu huku kiongozi wao akiwa moto zaidi. Kuna mahojiano yaliyokuwa yakiendelea kati ya askari huyo na mama mmoja. Sembuyagi akawa kimya zaidi ili kunasa chochote.




"....mimi nilikuwa nimechoka sana kwa kazi za mchana kutwa kama nilivyoeleza mwanzo hivyo nikaelekea zangu chumbani kulala huku mume wangu nikimuacha sebuleni akiangalia tamthilia ambayo alikuwa akiipenda sana akaniambia kuwa itakapokwisha ndipo angekuja kujumuika nami kulala." Alikuwa ni yule mama mtu mzima, mnene, mweupe kiasi mwenye sura pana na macho makubwa ya mvuto. Kwa maelezo yake, Sembuyagi na wenzake wakajua ni mke wa marehemu. Hawakutaka kusikia kwa mbali mahojiano hayo, walitaka kuingia ndani kabisa hata hivyo wakazuiwa.




"Hakuna ruhusa ya kuingia kwa sasa humu ndani kuna mahojiano baina ya askari na familia ya marehemu." Aliongea askari mmoja mdogo mweusi mwenye macho mekundu, umbo lake lilionesha kudumaa lakini akidhihirisha umri mkubwa kulingana na ukomavu wa sura yake.




"Tunahitaji na sisi kuyasikia hayo mahojiano yanaoendelea humo ndani," akajibu Sembuyagi akiwa bado anatazama ndani ambako yule mama na yule askari walikokuwa wakiendelea na mahojiano.




"Ninyi kama akina nani?" Akauliza yule askari mkomavu. Marietha hakusubiri, alichomoa kitambulisho cha kazi kutoka kwenye mfuko wake wa suruali na kumpatia. Yule askari akakitazama na kuwa mpole kidogo kisha akawageukiwa wale waliyopo mule ndani. Akawaamuru askari wenzake wapishe, Sembuyagi na wenzake wakapita.




"Unakumbuka ulikuwa ni muda gani wakati hao watu wanavamia?" Koplo yule akauliza akiwa anamtazama moja kwa moja usoni yule mama hata hivyo mwanamama huyo akashindwa kutoa majibu baada ya kumuona Sembuyagi na wenzake wakiwa hapo. Koplo akageuza shingo kutazama nyuma ndipo akapigwa na butwaa asilolitarajia.




"Ninyi ni wakina nani? Na kwanini mko hapa?" Akauliza Koplo pasipo kusubiri majibu kutoka kwa mwanamama yule. Mabule akajitambulisha kwa niaba ya wenzake kisha Sembuyagi mpauko haufi akamgeukia yule askari aliyekuwa akiendeleza mahojiano akamwambia.




"Tuko hapa kwa oda maalumu kutoka Ikulu hivyo usifikirie tofauti, hili si suala dogo kama linavyoonekana. Samahani sana kwa kuingilia majukumu yako japo tunaweza kushirikiana kupata chochote kutoka kwa mama huyu....!" Baada ya kusema naye akamgeukia mama yule.




"Mama, wewe ni nani kwa marehemu?" Aliuliza kujipa uhakika.




"Marehemu ni mume wangu."




"Unajua kwanini alivamiwa na kuuawa?" Akauliza Sembuyagi Mpauko Haufi.




"Hapana sijui sababu ya kuuawa kwa mume wangu...!"




"Mumeo hakuwa na ugomvi, kutokuelewana na majirani, marafiki, baadhi ya ndugu ama jamaa wengine au pengine alikuwa na ugomvi wa kimapenzi na mtu mwingine?" Akauliza swali Sembuyagi. Mke yule wa marehemu akalijibu kwa haraka kuwa mumewe hakuwa mtu wa namna hiyo.




"Ni mlevi?"




"Hapana."




"Hana matatizo ya kugombea mali na nduguze kama magari, nyumba na mashamba?" Akauliza tena Sembuyagi hata hivyo mwanamama yule alikataa. Sembuyagi akatulia na kujipa utulivu huku kichwani mwake kukipita mlolongo wa picha nyingi hasa kuhusiana na namna mauaji yalivyo, maswali yake hayakuwa na maana yoyote kwani mnyororo wa vifo hivyo hasa ulikuwa ukiwahusu viongozi. Vipi kuhusu maswali anayouliza? Si kweli. Walitakiwa kubadili namna ya kuuliza.




"Muda unaukumbuka wa tukio?" Mabule akatupa swali ambalo Koplo aliuliza na kuchelewa kujibiwa. Mwanamama akaingia kwenye tafakuri fulani kabla ya kujibu.




"Ni nusu saa baada ya tamthilia kuanza, ni kama saa tano na nusu hivi kaka!" Akajibu mwanamama huyo.








Walitakiwa kubadili namna ya kuuliza.




"Muda unaukumbuka wa tukio?" Mabule akatupa swali ambalo Koplo aliuliza na kuchelewa kujibiwa. Mwanamama akaingia kwenye tafakuri fulani kabla ya kujibu.




"Ni nusu saa baada ya tamthilia kuanza, ni kama saa tano na nusu hivi kaka!" Akajibu mwanamama huyo.




"Kuna majadiliano yoyote uliyasikia kabla ya kufanyika mauaji?" Akauliza swali la msingi sana Marietha hadi Sembuyagi akamtazama usoni.




"Ndiyo, mabishano yalikuwepo na hayakuwa marefu sana, kubwa lililokuwa likiulizwa ni kuhusu familia yake kama ipo, mume wangu alikataa kusema kama tupo. Pili ni....ninyi ni akina nani...? Swali hili lilitoka kwa mume wangu hata hivyo hakujibiwa na badala yake akaulizwa yeye kuwa ni kipi alichovuna baada ya kuisimamia kidete kesi ambayo hakujua madhara yake kwa mshitakiwa ni yepi?" Hapa sikumsikia mume wangu akijibu na badala yake alisema kuwa kila baya litalipwa. Nilipata mashaka sana na nikaamua kuchungulia kupitia upenyo mdogo wa mlango. Lo! Nilichokishuhudia sijawahi kuona, wale mabwana ni katili na wauaji hasa. Walimpiga risasi mbili, moja ya kifuani na nyingine ya kichwani mume....mume...!" Akashindwa kuendelea yule mwanamama akawa anatokwa na machozi huku akionekana kukabwa na dukuduku zito sana kooni. Likawa ni jukumu la kumpa moyo na kumtia nguvu ya uvumilivu. Walitaka aendelee zaidi kujibu.




"Hukubahatika kuziona sura zao?" Swali jingine kutoka kwa Marietha likamfikia mwanamama huyo baada ya kuyapisha machungu yapite kwa muda.




"Nazikumbuka sura zao...! Hapana, namkumbuka mmoja tu kati ya wote....!"




"Unaweza kumuelezea namna alivyokuwa?" Sembuyagi akauliza naye.




"Ndiyo, tena kwa ufasaha mkubwa maana yeye ndiye aliyekuwa kipaumbele kwa kila kitu hadi kumuua mume wangu, nilimuona kuanzia chini hadi juu na jazanda yake ilikaa machoni mwangu kwa ufasaha kabisa."




"Yukoje?" Akauliza akiwa na sura yenye tashwishi kidogo Sembuyagi huku mwili ukianza kumchemka kwa kile kilichokuwa kikizungumzwa hapo.


Kazi ilikuwa imeiva.




"Hapana kiongozi, tunatakiwa kuwa na picha halisi ya muuaji, hivi tutajiingiza kwenye mvurugano mkubwa sana na tutashindwa kupata vitu kwa wakati ni lazima tuwahusishe wataalamu wa michoro ili kuweza kupata uhalisia wa mtu anayezungumziwa hapa." Alishauri Marietha kuhusiana na jambo hilo kwani njia ya kumfikia muuaji ilikuwa rahisi sana kupitia maelezo ya huyo mama mke wa marehemu Masuka Mvungi.




"Hakuna mwengine ambaye amewaona wauaji hao?" Akauliza Sembuyagi akiwa makini zaidi sasa.




"Hapana, ni mimi pekee ndiye nilishuhudia kila kitu hadi watu hao wanaondoka." Jibu hili likampa wazo kichwani mwake akawatazama wenzake kisha akasema.




"Kwa sasa shughulikia masuala ya msiba, ifikapo kesho au leo jioni tutakuhitaji kwa ajili ya mahojiano zaidi nadhani tumepata ufumbuzi." Akasema Sembuyagi hata hivyo kauli yake hii ikawa nzito kueleweka kwa wenzake wawili hawa na kupelekea kuhoji kwanini isiwe ni muda huo na iwe ni jioni ama kesho. Sembuyagi hakuwa mjinga katika kutoa wazo ama kufanya maamuzi ya jambo fulani. Aliamini kabisa kama mwanamama huyu atapata muda wa kupumzika ni wazi anaweza kuwa na picha iliyotulia ya mtu huyo na ikawa rahisi kuielezea akiwa mbele ya mchoraji kuliko hivyo alivyo sasa.




"Kwasasa kichwa chake kimevurugika kutokana na kusumbuliwa na wanausalama mbalimbali wakitaka kujua sababu ya mauaji haya nadhani ni vema kama tukimpa muda mwingi wa kupumzika." Akasisitiza Sembuyagi Mpauko Haufi. Hapa wakawa wapole hata hivyo wakijiona kila wakati wakiwa nje ya muda.




Ikabaki kuwa kiongozi alishasema na kumpinga kiongozi ni kosa kubwa sana kwa askari wa aina yoyote yule au mwanausalama wa aina yoyote ile kiongozi akisema amemaliza na pia hoja yake kwa upande mwingine ilikuwa na mantiki makubwa, kilichobakia ni kusubiri oda. Wakaondoka hapo wakiweka kizuizi kwa askari waliopo hapo pia kuacha kuendelea kumuhoji mtu huyo. Polisi wakaondoka nao wakimuacha yule mama.




_________




Frank Matiale Bambi hakuwa nyuma kwenye hili naye, muda wote alikuwa akifuata matukio hayo mawili hatua kwa hatua. Hakuwa amewahi kufika kwenye matukio haya hata kidogo kwani kila anapofika anakutana na wanausalama na askari polisi wengi wakiwa wametanda. Hii kesi ya mauaji ilionekana kuwazidi nguvu polisi. Kwani kila wakutanapo na wanausalama hawa kutoka usalama wa taifa, huzuiliwa wasiendelee na zoezi lao na kigezo kikubwa kikiwa ni kwamba oda hiyo imetoka Ikulu moja kwa moja hata wakipeleka taarifa kwa viongozi wao wanakutana nazo hukohuko ikimaanisha kuwa ziliwatangulia. Pamoja na hayo pia kuna baadhi ya askari walihisi kuwa hiyo ilikuwa ni hoja butu, hoja isiyo ya kweli kwani hawakudhani kama amri kama hiyo iliweza kutolewa na viongozi wa juu. Ikawapa mshawasha wa kujiuliza maswali mengi ambayo majibu yake ni kwamba walitakiwa kuwa makini katika uchunguzi wao na na hasa ikiwa ni kufuata maagizo ya wakuu wao wa kazi.




Uchunguzi wa Frank kwa Kiago Mathias ulikuwa mgumu sana kwani kwa upande ule hakukuwa na shuhuda hata mmoja na wote waliokuwapo lindo waliuawa. Alijaribu kupita kwenye kamera za ulinzi nako hakuna alichokipata. Ilikuwa ni hali mbaya sana kwa upande wake. Hakukata tamaa aliongeza mbinu za uchunguzaji kupitia tukio la kwanza la mauaji lililotokea Sokoni hadi hilo. Hili lilikuwa tofauti na mauaji mengine. Muuaji huyu alionekana kuwa fundi wa kuuwa kwa kutumia mwili na silaha. Namna alivyowashambulia walinzi, namna alivyotumia akili kuwatoka polisi na namna alivyommaliza Jaji Kiago Mathias.




Huyu alikuwa fundi. Akajiwazia zaidi. Akaondoka hapo akiwa nyuma vivo hivyo akikubali kuwahiwa hadi kwenye nyumba ya Masuka Mvungi. Nako akawa nyuma ya wanausalama wengine. Akiwa ametulia garini mwake huku gari yake ndogo ikiwa katikati ya gari nyingine za watu waliyofika msibani, aliweza kufuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Aliwaona polisi walivyokuwa wakihangaika kupata japo chochote kutoka kwa wafiwa. Kuna jambo lilimvutia nalo ni namna vijana watatu walivyokuwa wakifanya kazi pamoja na kwa kushirikiana. Akawaza kwa muda na kuona akiendelea kukaa ndani ya gari ni wazi atapoteza lengo. Akateremka na kuchangamana na watu waliyofika msibani hapo. Kimya kilikuwa kikuu kwake na wazo la kuhakikisha anapata kitu likamungia damuni hasa. Aliwatazama vizuri watu wale watatu hakumjua hata mmoja na akili yake ikakili kuwa hakuwahi kuwaona mahali. Ungamo ilimuamini sana yeye na alikuwa akifahamu fika kuwa taifa hilo lilikuwa likitegemea juhudi zake. Akajiapisha kuwa lazima apambane kufa na kupona hadi kieleweke, palipo yeye huwa hapaharibiki kitu, hiyo ilikuwa ni zaiada ya imani yake. Hao walikuwa ni watu wapya kabisa machoni mwake kwa namna alivyowatazama japo kwa mbali sura ya binti yule ikiwa kama inajijenga kichwani mwake na kutoka hata hivyo alipochunguza zaidi akagundua wote wawili yaani yule binti na kijana mmoja walikuwa wakiongozwa na bwana mwenye kapelo na miwani myeusi kubwa machoni mwake. Hakuwa mvivu wa kuendelea kusubiri Frank, akawa msubirifu hadi pale alipoona wanaondoka. Hakutaka kujiridhisha kwa kutazama bali akifanya maamuzi yaliyosahihi, kwanza alichukua picha kadhaa za vijana wale kisha akasubiri hadi hali ilipotulia yaani hakuna watu wenye kuwatilia shaka ndipo akapiga hatua kuelekea ndani. Alipofika mlangoni akawasalimia aliowakuta kisha akauliza kama angeweza kumpata mke wa marehemu. Miguno ikasikika ya kutosha. Alitegemea hilo. Hii ilimaanisha fika kuwa mama huyo alikuwa hatulii kila mara ni mwenye kuhitajika, kuhitajika na yeye hata hivyo alioneshwa na kuambiwa aingie ndani kwani mama huyo hawezi kutoka nje. Frank kabla ya kuingia kwanza alitazama usalama wake akitaka kuangalia kama yupo wa kumfuatilia, alipoona hakuna akaingia ndani. Aliwaruka wakina mama kadhaa hadi alipoingizwa kwenye chumba husika ambapo alimkuta mama huyo akiwa amejiinamia kashika tama. Akamsalimia na kumpa pole kisha akajitambulisha kwa majina yake bandia na kutoa kitambulisho chake cha kazi cha kughushi pia. Akampa pole kwa masikitiko makubwa huku akijivika uchungu mkubwa usoni mwake.


Alimhurumia.




"Mumeo aliuawa kwa kupigwa risasi mbili, huwenda watu waliofanya hivyo walikuwa na dhamira thabiti kabisa ya kutaka kuua na si kuacha majeruhi, jambo hilo kutokea linajionesha kabisa kuwa si kwa bahati mbaya. Mara nyingi linapotokea hilo huwa kuna mambo kadha wa kadha yenye kusababisha na mambo hayo yanaweza kuwa; ugomvi, ulevi, wivu wa mapenzi ama vinginevyo. Je, kati ya haya yote niliyoyaorodhesha hapa ni kipi ambacho mumeo alikuwa nacho?" Akauliza Frank akiwa makini katika kumtazama mama huyo usoni. Alitaka kuona jinsi ambavyo angejibu. Macho yake yalikuwa makini kuliko ilivyo kawaida.




"Mume wangu hakuwa na tabia hata moja miongoni mwa hizo ulizo ziorodhesha hapo," alijibu mke wa Masuka.


"Siku za usoni hukumskia mumeo akizungumzia jambo lolote nje ya mazoea aliyonayo?" Akauliza tena Frank Matiale. Mke wa Masuka akapiga kimya kwa muda akitafakari kwanza kishapo akamtazama kijana aliyeko mbele yake.




"Hapana, hakuwa akizungumzia chochote kile mbali na nilivyomzoea."




"Wakati mauaji yanatokea, wewe ulikuwa wapi?" Mke wa Masuka akamtazama kijana huyo usoni kabla ya kujibu, akaona hakuna swali jipya bali kinachofanyika ni upindifupindifu wa maswali hayo. Akaeleza kila kitu kuhusiana na alivyoshuhudia.




"Unaweza kuniambia jinsi watu hao walivyo kwa jinsi ulivyowaona?"




"Si wote, mmoja tu ndiye nilimuona kwa ufasaha. Naweza kueleza namna alivyo."




"Yukoje?" Akauliza zaidi Frank Matiale Bambi. Mke wa Masuka Mvungi akavuta kumbukumbu kwa utulivu mkubwa, zilipita sekunde kadhaa ndipo akanyanyua mcho yake kumtazama kijana huyo.




"Ni mrefu mweusi, mwenye sura nyembamba, macho mekundu madogo, pua fupi iliyohifadhi tundu zake pana. Alikuwa na kidevu kirefu pia alikuwa na ndefu alizozichonga kiasi kama mzuzu hakuwa amevaa kofia yoyote kichwani.....!"




"Samahani kidogo mama, wacha nilifanye hili kitaamu zaidi." Akasema Frank kisha akatoa simu yake mfukoni na kutafuta jina fulani simuni mwake kishapo akaiweka sikioni.




"Ndiyo mtaalamu, habari za majuma kadhaa?" Akasalimia akatulia kidogo kupata mpokeo kisha akaendelea.




"Ni majukumu ndugu yangu hakuna la zaidi," akaweka koma tena, baada ya mpokeo kurejeshwa akasema.




"Sawa sawa, sasa...nawaze kukupata kwa muda gani hasa kuanzia sasa maana niko na kazi ambayo itahitaji zaidi uwezo wako?" Akaweka sikio vizuri kwenye spika ya simu kupata mrejeo kwa usahihi.




"Ok, nashukuru ni muda huu nakuja kwani linahitaji uharaka mno na sitapenda kukawia." Akahitimisha kisha akairudisha simu mfukoni mara baada ya kuikata. Akamgeukia mjane yule akamtazama kwa tuo mithili ya mtu apangaye jambo la kumwambia. Haikuwa vinginevyo. Akashusha pumzi kisha akasema.




TUTASONGA.








"Ok, nashukuru ni muda huu nakuja kwani linahitaji uharaka mno na sitapenda kukawia." Akahitimisha kisha akairudisha simu mfukoni mara baada ya kuikata. Akamgeukia mjane yule akamtazama kwa tuo mithili ya mtu apangaye jambo la kumwambia. Haikuwa vinginevyo. Akashusha pumzi kisha akasema.




"Mama mimi pekee ndiye mwenye kuweza kukufikisha mahali ambapo utapata kuhakikisha walio tenda mabaya kwa mumeo wanaingia mikononi hakikisha hili linakamilika na haliwezi kukamilika kama hutanipa ushirikiano wako wote," akaweka koma na kumtazama mjane huyo. Mama akasema kuwa ni furaha yake kuona waliotenda hayo wanaingia mikononi mwa sheria na pia sheria inachukua mkondo wake dhidi yao.




"Lazima mimi nawe tuondoke sasa hivi hadi kwa mtaalamu wa masuala ya michoro ili ukahadithie namna unavyomjua muuaji kwa ulivyomuona. Hakuna namna nyingine ya kuweza kuwakaribia wauaji kwani hapa hakuna ulinzi wa kutosha ambao angalau ungetupa mwangaza." Mama akatulia kwa kitambo kidogo akijishauri nafsini mwake. Mwisho wa hayo akakubali japo kwa shingo upande. Mama yule akaaga kwa watu wake muhimu na akisema kuwa atarudi baada ya muda mfupi ujao. Wakatoka hadi garini. Kijana huyo akawasha gari na kuondoka.



ITAENDELEA


imulizi : Mpango Wa Nje - Ni Pigo Butu La Kifo 


Sehemu Ya Nne (4)




Walipita kona hii na ile wakazifuata barabara kadhaa na kushika chochoro hii na ile wakaja kutokea nje kidogo ya mji. Frank Matiale Bambi akatafuta maegesho ya muda akaegesha gari na kutoka akamfungulia mama yule mlango na kutoka. Waliweza kuongea mengi wakiwa ndani ya gari hivyo hadi kufikia hapo walikuwa wakiongea kama marafiki huku Frank akiwa ameshamfahamu mama huyo kwa majina yake.




"Binti Mbaruku usiwe na wasiwasi kabisa hapa ulipo uko salama na utaendelea kuwa salama. Ninachokihitaji ni wewe kuwa muwazi kwa kile unachokijua," akasema Frank. Binti Mbaruku mke wa Masuka Mvungi akaitika kwa kutikisa kichwa kichwani mwake alionekana kuwa na mafikirio makubwa sana huwenda jazanda la mauaji ya mumewe lilikuwa likimsumbua kwa kiasi kikubwa mno.


Alikuwapo kama hapo.




Hatua za kuhesabu zikawafikisha kwenye jengo moja ambalo kwa nje lilikuwa na ofisi moja ambayo kwa juu ya mlango ilipambwa na maandishi makubwa ya kupendeza. Mchoraji. Wakaingia ndani ya ofisi ile kwa kulitawanya pazia la urembo la kutungwa kwa vikoa vidogodogo na nyuzi maalumu.




"Karibuni sana." Mtu mmoja aliye nyuma ya meza kubwa iliyojaa vifaa mbalimbali vya kuchorea kama rangi, peni, penseli, karatasi ngumu na nyepesi, visu, viwembe na kadhalika. Juu kwenye kuta za pande zote kulipambwa na picha za aina mbalimbali za kubuni ambazo zilivutia sana kwa kuzitazama.




"Asante sana M.D naona michoro inazidi kuita ndugu yangu?" Akaitika ukaribisho ule Frank Matiale Bambi akiwa bado anaikagua ofisi ile.




"Ndiyo, ndugu yangu...nikasema leo sibanduki hapa hadi nikuone maana huonekani kihasarahasara, haya nipe hiyo kazi mikono bado ina nguvu sijafanya chochote hivyo natumai nitakutolea kazi nzuri." Alijinadi M.D huku akiacha alichokuwa akikifanya na kuwatazama kwa zamu wateja hao. Frank alimkaribisha kiti Binti Mbaruku. Akaketi naye akatwaa nafasi akaketi kishapo wakaingia kwenye kilichowafikisha hapo.




Mvua ndogo ndogo ilikuwa imeanza kunyesha huko nje hata hivyo haikuleta usumbufu kwenye kazi hiyo. Binti Mbaruku akaeleza kila kitu kuanzia ukucha hadi unywele. Kazi ilikuwa ikifanyika hatua kwa hatua hadi kufikia tamati. M.D aliyekuwa amejiinamia kwenye dawati lake la kazi hata alipokuja kuinyanyua sura yake, akaitua sambamba na picha moja mezani. Alipoiweka tu picha hiyo mezani Binti Mbaruku akashtuka mithili aliyeona kitu cha kutisha mbele ya macho yake.




"Vipi?" Akauliza kwa hamaki Frank Matiale Bambi.




"Ndiye mwenyewe hivi hivi hakuna utofauti. Ndiye huyu muuaji wa mume wangu." Alisema Binti Mbaruku kwa kupayuka hata hivyo kauli ile ya kusema kuwa yule pichani ndiye aliyemuulia mume wake, ikamfungua masikio M.D akajua kuwa huwenda picha hiyo ikawa ni dili kubwa kuliko alivyodhani yeye. Kumbe mtu aliyemchora ni muuaji? Alijihakikishia kiasi kikubwa sana cha pesa kama kungetokea mtu mwingine na kuihitaji. Frank aliichukua ile picha na kuitazama kwa umakini mkubwa hata hivyo hakuwa amepata kumbukumbu zozote kama mtu wa namna hiyo aliwahi kukutana nae mahali.




"Asante sana M.D kwa kazi nzuri, unatakiwa kuwa makini sana na hili maana picha hii ni ya mtu hatari mno." Akasihi Frank kisha akamkabidhi kijana huyo shilingi elfu hamsini. Kijana huyo akashukuru sana kwa kupewa kiasi kile cha pesa kwa kazi ambayo haikumuumiza hata kichwa sana. Si kama hakuwa akipata pesa nyingi la hasha! Alizipata ila ni kwa watu wachache wenye kuijua thamani ya michoro. Hii ilikuwa ni asubuhi njema kwake na aliamka na nguvu kubwa. Frank na mama mjane Binti Mbaruku walitoka nje wakatembea ndani ya mvua hiyo ndogondogo. Hadi garini. Kilikuwa ni kipindi cha Mchoo hivyo mvua za namna hiyo zisizo tabirika lilikuwa ni jambo la kawaida. Alimrudisha hadi nyumbani kwake akamtaka umakini na kutokusema alichokifanya naye. Wakakubaliana na kijana huyo akaondoka.




___________




Bado niliendelea kusumbuliwa na jazanda la mtu yule mwenye mavazi meusi ambaye alitenda mauaji yale, fikra zangu zilikuwa zikinituma mengi ya kufanya hata hivyo sikujisukuma kuyafanya. Mengi yalikuwa ni kuhakikisha nafuatilia nyendo za mtu huyo hata hivyo suala la kujiuliza ni je, naanzia wapi kumfuatilia mtu huyo? Pili, ni kujua kwanini ameua au kwanini anaua? Hili nalo lilikuwa gumu kwa kuwa muuaji sikumjua undani wake, nalo hili lilitegemea suala la kwanza ndipo hili lijibike. Ukweli ni kwamba jibu lilikuwa gumu kwa kuwa swali la kwanza lenyewe lilikuwa mtihani kulijibu, vipi la pili?




Nilipiga muayo mrefu sana uliombatana na kite cha uchovu. Bado nilikuwa nawaza namna ya kufanya. Nadhariatete ikaundika kichwani mwangu, hii sikuipuuzia nikajipa muda kisha nikaidadavua na kupatia maamuzi mazito ambayo kwa kazi yangu niliamini yangenifikisha nipatakapo. Nikaitazama saa yangu ya mkononi ilikuwa tayari muda umekimbia. Nikapiga muayo mwingine nikajua nini sababu ya hali hiyo. Sikuwa nimelala usiku wote uliopita nikimfikiria muuaji niliyepambana naye na kunikimbia pasipo kumtambua hata nywele yake, nakuja kutahamaki hammadi! Alfajiri usoni. Muda ulikuwa unaniruhusu kufanya kazi niitakayo na kwa kuwa muda ulikuwa umekwenda nilijisahaulisha kula kwa muda kisha nikajitoa ndani na kuelekea mahali ambapo niliegesha gari yangu. Jawabu ni kwamba muayo na kite kisichokwisha ni cha uchovu na njaa. Sikujali sana bado, nilijipa upofu wa kusikia na uziwi wa kulitazama tumbo namna linavyoporomosha mashairi yasiyo na vina elewevu na mizani pindifu. Njaa ni mwanaharamu ila nilijivika mkaja wa maumivu wa kujitwisha vidonda vya tumbo kwa hiyari. Sikutaka kula kwa wakati huo. Mashine ya Peugeot 404 ikaitikia kwa kishindo cha kunipa mzuka wa kuingia barabarani, hii ni baada ya kuiwasha gari yangu. Nilizidi kuipasha moto injini hadi nilipojiridhisha kisha nikaliondoa hapo taratibu kuingia mitaani.




Muda ulikuwa ukienda kwa kasi ya umeme kiasi kwamba siku nazo zikashindwa kukosa muhimili na kujikuta zikikimbia kwa kasi ileile. Ni majuma kadhaa yamekatika tangu kuwa ndani ya jiji hili la Muavengero na hadi sasa nilikuwa bado sijafika kwenye chanzo cha kazi yangu. Sikujua huyu mtu wa kuitwa Musa nitampata kwa namna gani na pia sikujua nitaanzia wapi kumuulizia na nilipofikiria hilo na yale maneno ya AKM ya kunitaka nifanye kilichonileta yakanijia kichwani. Nikaona huwenda ninachokifuatilia pia hakikuwa kwenye jukumu langu hata hivyo sikuwa na namna ya kufanya nililazimika kufanya hivyo na sikupaswa kusimama kwani nilijipa uhakika wa kufika nipatakapo. Nilikuwa nikikanyaga pedeli ya mafuta huku macho yangu yakiwa makini barabarani. Kichwa kilikuwa kikiyarudisha matukio kadha wa kadha yaliyopita nyuma. Akili yangu ilikuwa ikigoma kufunguka kila nilipokuwa nikiifikiria safari hii.




Nini nimefanya na nini nafanya....? Hah hah haaa...! Nilijikuta nikijichekesha mwenye garini kama mwehu huku nikijiuliza maswali yasiyoeleweka kama yanafaa kujiuliza ama la! Na yote hiyo ni mara baada ya kujikuta niko ndani ya pigo butu la kifo. Muuaji simpati na watu wanaoonekana muhimu wanakufa.




Kwanini wafe? Nikajiuliza nikiwa nakunja kona moja, sasa nilikuwa nimeikaribia nyumba ya marehemu Masuka Mvungi kwa taarifa nilizozipata kupitia vyombo vya habari, zilisema kwamba mtu huyu aliuawa kwa kuchapwa risasi mbili ambazo zilibeba uhai wake. Nikaliunganisha hili tukio kwenye nyororo yangu ya uchunguzi wa kupata njia. Swali nililojiuliza sikuwa na jibu nalo na ni kama niliidandishia gari kwa mbele akili yangu.




Nilisimamisha gari kwenye uwazi fulani huku nikitembeza macho yangu kwa umakini nikitafuta mahali pa kuegesha gari yangu ili niweze kufutatilia kitu kimoja baada ya kingine. Wakati nikiwa hapo, niliona gari za polisi mbili Land Rover Deffender moja na Toyota Mark II ambayo ilikuwa na kimulimuli kwenye paa lake. Sijakaa sawa, gari nyingine ikapita hii ilikuwa ni Noah yenye rangi ya maziwa ikiwa na vioo vya giza. Sikuhangaika nayo sana haya magari bali nilichokifanya ni kuliondoa gari langu hadi kwenye maegesho niliyoyaona ambayo yalisaliwa na magari saba yenye hadhi tofautitofauti. Nikajipenyeza katikati na kupachika gari yangu hapo hata hivyo sikuteremka bali niliganda hapo nikitazama hali halisi ya eneo hilo. Nilitulia kwa kitambo kidogo, na nikiwa nazidi kuweka utulivu huo, kwenye dashibodi ya gari yangu nikaona sigara ambayo nakumbuka niliitelekeza hapo siku ambayo nilikuwa nikizifuatilia gari mbili zilizokuwa zikifukuzana ambazo muishilizio wake ulisababisha kifo cha yule mzee. Niliihurumia sana sigara hiyo kwa kukaa hapo kwa muda mrefu bila kutumika. Nikaichota na kuipachika kwenye kingo zangu za midomo kama mvutaji mbobezi kumbe nilikuwa mvutaji mchwara tu pengine nisiyeyajua madhara ya uvutaji wa sigara kiundani maana hata maandishi ya onyo la uvutaji wa sigara niliyaona kama yanayonibashiria uvutaji mwema wenye amani hadi mbinguni.


Makubwa!




Ama kwa hakika hizi zilikuwa ni vurugu za dagaa kupambana na kokoro na ilhali hana ujuzi wa kujinasua. Nikaiwasha sigara yangu kwa kiberiti cha gesi na kukitupia kwenye dadhibodi nikapiga pafu kubwa na kupulizia moshi nje. Nilivuta mivuto kama mitatu kisha nikaibana kwenye pacha ya vidole vyangu vema na kutazama watu wote waliyokuwa wamekaa mahali ambapo palikuwa na viti vingi kwa ajili ya waombolezaji mbalimbali. Nikiwa natazama kwa jicho langu makini, nilimuona mtu ambaye nilianza kumtilia shaka miongoni mwa watu wote walioko hapo. Nikaweka utulivu wa macho yangu huku nikiivuta tena sigara yangu kwa pafu la wastani.






Nikiwa natazama kwa jicho langu makini, nilimuona mtu ambaye nilianza kumtilia shaka miongoni mwa watu wote walioko hapo. Nikaweka utulivu wa macho yangu huku nikiivuta tena sigara yangu kwa pafu la wastani. Huyu hakuwa mtu wa kawaida. Alikuwa amevaa miwani myeusi hata hivyo baada ya muda akaivua na kuiweka kwenye mfuko wa shati lake. Nikazidi kumtazama. Nikamuona akiizungusha shingo yake kushotoni na kuumeni, sikuwa na shaka kwani gari yangu ilikuwa sehemu ambayo hata kama angeangalia kwa namna gani asingeliniona. Akasimama na kupiga hatua hadi kwenye mlango wa nyumba yenye msiba. Akatazama tena nyuma kwa mtazamo uleule hapa nikaiona sura yake vizuri alikuwa jamali, mwenye umbo la wastani hakuwa mfupi wa kutisha wala njorinjori, alikuwa amevaa shati la mirabamiraba lenye mikono mirefu. Chini alivaa kiatu cha rangi nyeusi safi kilichomkaa vizuri. Nikauhifadhi muonekano huu kwenye memori yangu ya kumbukumbu kichwani, nilijiamini katika kushika mambo kwa haraka sana na hii ndiyo sifa pekee ambayo najivunia nayo kwa kiasi kikubwa tukiachana na nyingine nilizotunukiwa na muumbaji wa mbingu na ardhi. Nilipoteza muda nikimsubiria atoke mule ndani ili nijue nini nifanye dhidi yake. Nikaendelea kuvuta sigara yangu taratibu huku jazanda ya vitu na mambo kadhaa yakija kichwani mwangu. Nilimkumbuka yule kijana niliyekutana naye kwenye basi chakavu wakati nikiwa naelekea kwenye kijiji cha Asumile ambaye alijitambulisha kwangu kama Jamali Maigwa. Nikatabasamu baada ya majuma kadhaa kukatika bila kupata simu yake wala ujumbe mfupi wa maneno kutoka kwake.




Huwenda ni mtu wa maneno mengi lakini domo zege. Nikawaza huku nikizidi kutabasamu sigara nayo ikiendelea kuteketea. Nikaachana na wazo hilo baada ya jambo la muhimu na msingi mkubwa kunijia kichwani mwangu. Nalo ni kuhusiana na kijana niliyemuona akiingia kwenye nyumba yenye msiba.


Niliwahi kumuona mahali.




Kumbukumbu hizi ziliutafuna ubongo wangu na kuliacha fuvu la kichwa likiwa kavu na mafikirio yake. Nikapiga vidole vyangu kwenye dashibodi ya gari yangu na kuzipeleka kwenye uchanganuzi kumbukumbu hizi. Naam! Nilikumbuka.




"Nilikutana na huyu mtu sokoni kwenye tukio la mauaji ya Kamanda Mansuli Bingwa." Nikajisemea baada ya kukumbuka. Hapa nikavuta pafu refu sana la sigara yangu na kujikalisha vizuri kitini.




Alikuwa akilichunguza gari la marehemu punde tu baada ya kutokea mauaji. Niliwaza. Sasa nikajua mbele yangu niko na mpelelezi. Huyu lazima atanipeleka ninapopataka na sitamuacha. Nikaendelea kutulia.




Nikiwa hapo bado huku sigara nayo ikiwa imekwisha, nilikitupa kipisi nje huku mbele yangu nikimuona Yule kijana na mwanamama mmoja wakitoka ndani ya nyumba ile ya msiba. Kwa jinsi alivyo yule mama akili yangu ikafanya kazi ya haraka kuwa bila shaka atakuwa ni mke wa marehemu Masuka Mvungi na si vinginevyo, kuna kitu nilikiona ni jinsi muonekano wake ulivyo, nikajiweka sawa kwenye usukani huku nikitoa PK mfukoni na kuanza kutafuna baada ya kuimenya. Macho yangu yakamshuhudia yule mama na yule kijana wakiingia kwenye gari baada ya yule mama kuaga kwa wazee wawili akiwa na yule kijana. Gari ikawashwa na kutolewa eneo hilo nami nikatafuta namna ya kuondoka kuwafuatilia bila kuacha maswali nyuma wala kwa wafuatiliwaji. Kwa kuwa nilijua aliyepo mbele yangu ni mpelelezi hivyo nilitumia akili sana katika ufuatiliaji wangu kwani sikutaka kufanya makosa hapa pia. Magari mawili yaliyonitangulia yakawa ni ukingamo tosha wa kunikinga nisiweze kuonekana. Nilizidi kuwafuatilia huku nikijenga maswali mengi kichwani mwangu ni wapi wanapokwenda? Pamoja na kujiuliza hata hivyo nilizidi kuwa mvumilivu wa ufuatiliaji wangu kwao. Tulipofika mbele ile gari niliyokuwa nikiifuatilia ikaingia kushoto na kuifuata barabara ndogo ya kichanga, ikayoyoma nami nikiwa mbali nao nyuma yao vivo hivyo. Nilikunja kona ile na hii, hii na ile hadi nilipoona wameegesha gari yao mahali nami nikatulia hapo nikiwatazama nini watafanya. Waliteremka na kutoka garini kisha wakapita kwenye uwazi wa nyumba mbili, nikatazama ni wapi naweza kuitelekeza gari yangu kwa muda kidogo. Nikaona hapo nilipo ni mbali sana kama nikiamua kutaka kuwafuatilia tena. Nikasonga mbele na kuiacha gari yangu kwenye uwazi fulani ambapo ni kama palikuwa na uwanja wa kuchezea watoto wadogo nyakati hizo za jioni kwa kuwa siku hii kulikuwa na manyunyu ya mvua makubwa huwenda ikawa sababu ya kutokuwepo ene lao la michezo. Nilikuwa na imani kubwa kuwa haitashtukiwa kwa namna nilivyoiegesha. Mara nyingi kipindi cha mchoo kifikapo, watoto huwa wavivu sana kucheza maana mvua zake huwa nyepesi zisizokoma haraka. Nikateremka na kufunga gari yangu vizuri nikajiweka sawa kwa kujifunika na mtandio kichwani japo nilivaa suruali ya jeans na fulana nyekundu chini nikiwa nimepiga simple raba. Nilisonga sasa nikiwa nimewakaribia na hawakunitilia shaka kwa kuwa nilikuwa kama mpita njia tu kama wao. Niliwaona wakielekea kwenye ofisi moja ambayo juu ya mlango nilipoisoma nikajua kuwa ilikuwa ni ofisi ya mtaalamu wa michoro mbalimbali. Hapa nikatabasamu moyoni mwangu kwani nilijua nini kilikuwa kikienda kufanyika. Sikutaka kuzubaa nikayazunguusha macho yangu haraka pembeni upande wangu wa kushoto kulikuwa na Saluni ya kike. Nikaona hii ingenifaa zaidi kwa kuwa nilikuwa na uwezo wa kufuatilia kila kitu nikiwa hapo kwa kuwa Saluni hiyo ilitazamana na ile ofisi ya mchoraji. Nikaifuata Saluni na kuingia ndani.




"Habari zenu warembo?" Nilisalimia, kulikuwa na wasichana wawili wazuri mmoja akiwa anaziosha nywele za mwingine. Waliitikia na kunitazama wakanikaribisha.




"Hapo tayari shosti, zifute kidogo na hicho kitambaa kisha utakaa pale kwenye Draya, wacha nimsikilize mteja....karibu dada?" Aliongea dada mmoja mrefu mwembamba aliyejaaliwa urembo ndani ya rangi yake nyeusi ya mvuto, akaongeza na ukaribisho.




"Asante, naweza kupata huduma au uko na mteja mwengine?" Nilimuuliza yule dada.




"Hapana, huyu ni wa hapahapa hivyo hana haraka, hata kukitokea mteja mwingine inabidi atoke pale kwenye Draya na amuhudumie mteja." Akasema, tukacheka nikakaa kwenye kiti ambacho niliamini ningeweza kuangalia kitakachokuwa kikiendelea kwenye ofisi ile ya uchoraji.




"Nataka kupunguza kucha na kubadili rangi maana ni muda sasa tangu niweke hii rangi," nikasema hitaji langu.




"Mbona bado zinaonekana zinadai, je, tunaweza kuweka kucha za kupachika ambazo ziko imara na zinazoendana na urembo wako?"




"Hapana, nataka kupunguza za mkono huu wa kuume lakini za kushoto zitabaki kama zilivyo kitakachoongezeka ni kutoa rangi hii na kuweka nyingine." Nikaelekeza. Kazi ikaanza huku soga za hapa na pale za kike zikiendelea. Niliwapenda kwa namna huduma ilivyokuwa nzuri na wanavyoijali kazi yao. Mikono ya dada huyo ilikuwa myepesi sana. Sikuwa mtu wa kupiga soga za umbea sana hivyo nilipoona soga za namna hiyo zinazidi nilibadili mada na kutumbukiza ya kwangu.




"Dada samahani, napenda sana picha za kuchora yaani nikae kwa pozi nilitakalo halafu mtu anichore huwa nafarijika sana na nikijiona kwenye mchoro huwa najiona niko halisi zaidi," nilichomekea huku nikisikiliza wadada hao wataongea nini.




"Hapa umefika bibie," dada yule wa kwenye draya akaongea.




"Unaona huo mlango unaotazamana na hii ofisi yetu?" Akaongeza.




"Ndiyo," nikajibu.




"Huyo ndiye mchawi wa michoro, kasomea huyo jamaa, watoto wa kike warembo wanamalizwa hapo na huyo jamaa maana muda mwingine hupata dili la kuwachora walimbwende wakiwa nusu utupu kitandani. Ni fimbo ya karibu huyo mshikaji na anajua kuua nyoka maana hupiga utosini." Maneno yalimtoka mtoto wa kike huyu aliyekuwa akinitengeza kucha si haba, nikatabasamu na roho yangu. Akaendelea.




"Hii michoro ya Saluni yetu amechora yeye kwanza hana bei ni mtu poa na msondani sana huyo kaka nampenda bure kwa kweli....!"




"Shostii! Nawe kakuchora picha ya chumbani nini maana unavyompa heko!" Yule dada aliyeweka kichwa chake ndani ya draya aliuliza baada ya huyu anayenitengeneza kucha kuonekana kumsifia sana huyo mchoraji.




"Tee! Walaa! Hajanichora picha ya chumbani, miye namsifia kutokana na vitu vizuri anavyovifanya hata hivyo tusiende mbali, wewe akikutaka utakataa?" Akasema dada aliyekuwa akinichora kucha.




"Aka! Mwenzangu nina kipenda roho changu bibi wewe, siwashwi na upupu, chupi kavuu haina harara, mkono wa jirani wa kunikuna wa nini!" Akabwata yule dada wa kwenye draya kisha akachomekea kwa huyu anayenipaka rangi za kucha.




"Wewe vipi mwenzetu?"




"Ebo! Anyimwacho mtu kitu....? Haramu yafichwa, ulichotunukiwa mtunukie mwengine bora tu akitendee haki, namtaka hata leo bado namvutia muda....!"




"Hehe heeee! Mwenzako ataka mbona hushtukiii...!" Akacheka cheko la kishakunaku yule wa kwenye draya kisha akaongezea.




"......shost tafuta Gest ya kumsaulia hayo yameshafika kwa havinitoshi." Cheko kubwa liliachiwa na dada aliye kwenye draya hadi nikahisi ngoma zangu za masikio zikitikisika. Kweli hii ilikuwa saluni ya kike. Ukitoa hili ukisema hawatalipamba kumbe ndiyo umewapeleka jikoni. Hata nia ya kuuliza ilinitoka hata hivyo yule wa kwenye draya pasipo haya wala soni akaniuliza.




"Dada unataka michoro?"




"Ndiyo, lakini uwe bora si bora mchoro," nikamwambia.




"Basi umefika, huyo ni fundi nisikufiche na ulivyo mrembo Mashaallah!....!" Akazidi kuchomekea huku akiiacha mwisho sentensi yake ikining'inia kumuacha msikilizaji amalizie mwenyewe.




Wakati soga zikiwa zinaendelea na shughuli ya kupambwa kwa kucha ikiwa imefikia tamati, nikawaona wale niliyokuwa nikiwasubiri wakitoka kwenye ile ofisi. Nikawatazama vizuri hasa yule kijana ambaye sura yake kwa hapo niliiona vizuri na kwa ukaribu wa kuweza kumsanifu. Alikuwa mzuri si haba, nywele zake za rasta alizozifunga nyuma na jinsi zilivyokuwa nyeusi, alinivutia kwa kweli, nilimuona kwa ufasaha kwani pazia la mlango wa Saluni niliyopo lilikuwa ni shanga nene ndefu. Nilimuona wa pekee sana na alinivutia kumtazama. Walitoka na kuelekea kwenye njia ambayo walijia. Manyunyu ya mvua yalikuwa yameshamiri vibaya mno. Nililipia nilichotakiwa kulipia kisha nikawaaga na kuwaambia naelekea kuchorwa na mimi. Wakacheka huku yule anayekausha nywele zake kwa draya akiniambia niangalie nisije kunasa. Nikajikuta nikitabasamu tu pasipo kumjibu chochote. Nilifika kwenye mlango wa ofisi ile nikapenya kwenye lile pazia la kiasili za vikoa na kuzama ndani. Nilimkuta kijana mmoja ambaye hakuwa mzuri wa sura pia hakuwa mrefu wala mwenye umbo la kunishawishi. Nikajua sababu ya 'kushobokewa' kwake na warembo ni namna anavyokitendea haki kipawa chake. Nilimkuta akitazama kitu fulani akiwa kwenye dawati lake la kuchorea, ni picha na niliiona kwa uchache sana kwa macho yangu makali na ya kidadisi, ilikuwa ni picha ya mwanaume aliyevaa fulana nyeusi ya mikono mirefu iliyomkaa vizuri, alikuwa na mzuzu alioufuga vizuri kidevuni. Sikuona kingine kwani aliwahi kuificha. Kilicho nichemsha damu ni jinsi kijana yule alivyoifutika picha ile kwenye mtoto wa dawati lake. Hakujua kama nimeiona nami kwa kuzuga niliyagandisha macho yangu kwenye kuta za ofisi ile. Niliona picha za wanyama na vitu vingi vya kijadi kama makabila maarufu ya nchi hiyo, Samaki wanaopatikana kwenye maziwa na bahari ya pwani za nchi hiyo, Milima maarufu ya nchi hiyo. Mawe mwakubwa ya msitu mkubwa na wa ajabu wa Dabaa Lonzo pamoja na picha ya kijiji kilichotikisa kwa maajabu yake ya kuogopesha, kijiji cha Indani chenye historia iliyojificha. Kulikuwa na picha nyingi ukutani. Picha za walimbwende, watu waliyochorwa na kupenda picha zao zibaki hapo kama 'sample' kwa watakaopenda kuchorwa namna hiyo.




MCHUNGUZI UCHUNGUZINI.






Mawe mwakubwa ya msitu mkubwa na wa ajabu wa Dabaa Lonzo pamoja na picha ya kijiji kilichotikisa kwa maajabu yake ya kuogopesha, kijiji cha Indani chenye historia iliyojificha. Kulikuwa na picha nyingi ukutani. Picha za walimbwende, watu waliyochorwa na kupenda picha zao zibaki hapo kama 'sample' kwa watakaopenda kuchorwa namna hiyo. Nilipoangalia nyuma ya kiti chake yaani ukuta ambao kiliegemezwa kiti chake, kulikuwa na picha kubwa juu ya kichwa chake yaani ni kama rula mbili kutoka kichwa kilipoishia hadi picha hiyo ilipo. Nilitabasamu kwa kuwa niliona utundu halisi wa kijana huyu kupitia ile picha. Sikusita kuuliza, uongo dhambi.




"Hii picha ni wewe ndiye ulichora au kuna mtu alikuchora?"




"Ni mimi!" Alinijibu kifupi akitabasamu.


Nilipenda.




"Uliwezaje kuchora hii?" Nilimuuliza tena huku nikiwa na lengo la kujua ni mtu wa aina gani na nitamuingizaje mahali nipatakapo. Sikuwa na tabia ya kukurupuka na hii ilinipa matokeo mazuri mno.




"Niliichora nikiwa nimekaa hapa hapa, ukiangalia hiyo picha ya Nyegere ambayo nimeigemeza kwenye huu mkebe wa vitendea kazi, pia kuna picha moja utaiona imelala juu ya hili dawati ni picha ile pale ukutani (akasontesha kidole mahali picha ilipo). Ilikuwa ni picha ya mhunzi wa kikoloni.....Picha hii niliichora kwa kutazama jazanda yangu kupitia kioo hicho hapo nyuma yako," nilistaajabu aisee! Huu ulikuwa ni uwezo wa aina yake. Nilipotazama namna picha ilivyo nikajua hakika kila kilichozungumzwa kilikuwa ni ukweli mtupu. Niliyazunguusha macho yangu kwa mtindo wa kike kike huku kwa namna fulani nikiyarembua na ilhali nikijua kuwa kijana huyo alikuwa akinitathmini kuanzia chini hadi kifuani. Nikapata wazo.




"Unachora picha za namna gani...? Mtu na rafiki yake, mpenzi wake wakiwa pamo, mtu mmojammoja au kwa namna gani?"




"Vyovyote vile nachora bora iwe ni vile mteja anataka," alijibu.




"Unataka kuniambia hata hawa wateja waliyotoka sasa ulikuwa ukiwachora au ni mtu tu amemleta mtuwe?" Niliuliza kwa mchomeko wa kutaka kumleta kwenye maana yangu huku nikiwa natazama ukutani.




"Hapana, hawa kuna kazi iliwaleta, inahusiana na michoro ha hivyo ni kazi ambayo haikuhusiana na picha zao wenyewe."




"Ok, kuna picha nimeiona ulikuwa ukiitazama, naweza kupata kubwa isiwe ndogo kama hiyo lakini mtu awe huyo....? Iwe kubwa ambayo naweza kuiweka chumbani kwangu, huwa napenda wanaume waliovaa 'simple' kama picha ambayo nimeona ukiiweka kwenye mtoto wa dawati lako?" Nilimuona huyo kijana akishtuka baada ya mimi kusema hivyo kisha akajichekesha kuupoteza mshtuko wake hata hivyo sura yake ilibakiwa na tashwishi fulani.




"Hapana.....hapana dada, hii ni picha ya mtu na anaweza kuifuata muda si mrefu." Akanijibu. Nikataka kumuomba niione bado nikajishauri nisifanye hivyo. Nikafikiri kwa muda kisha nikavuta kiti na kukaa naye karibu.




"Watu walioingia hapa ni watu ninaowafahamu hasa yule mwanamke, huyu mwanaume si sana....!" niliongea huku nikimtazama, nilimuona jinsi alivyonitolea macho utadhani ameona chuchu ya dhahabu juu ya titi langu moja. Nikajua ipo namna na ninakwenda kuijua. Nikaendelea.




"....yule mwanamke ni dada yangu, mumewe ameuawa kwa kupigwa risasi na watu wasiyofahamika, nilimshauri sana kuhusiana na kufanya upelelezi wa kifo hiki na kumwambia kuwa inaweza kuwa ni hatari kwake kwani katika kipindi hiki kila mtu anataka kujua ilikuwaje. Pengine wanaokuja kumuhoji ni watu walewale waliotekeleza mauaji, je, unamfahamu huyu kaka aliyekuja na dada yangu hapa maana nahofia asije akawa matatani kwa kijifanya yeye ni afisa usalama kumbe ni walewale?" Niliamua kubadili mtindo wa kuhoji mazima na nilikuwa na maana kubwa mno kwenye mtindo huu. Nilitaka kuuwa ndege wawili kwa jiwe moja maana Nyani mkongwe hafi kwa mshindo wa bunduki. Nilijua.




"Namfahamu!" Akanijibu M.D kama nilivyofahamishwa na wale wadada wa Saluni na pia jina hilo lilikuwa juu ya picha aliyojichora mwenyewe. Nikamtazama usoni nikagundua kuwa alikuwa ni mvutaji kama siyo wa sigara hizi za kawaida basi ganja. Nikayazungusha macho yangu pale juu ya dawati sikuona ninacho kihitaji, nikayahamishia kwenye meza nako sikuona kingine zaidi ya vitendea kazi vinavyohusiana na kazi yake, nikatazama vizuri ndipo nikaona chini ya karatasi moja kulikuwa na kiberiti cha kasha chenye nembo ya moto. nilikiona kwa uchache sana maana kilifunikwa nusu na ile karatasi. Nikamkagua yeye mwenyewe ndipo nikaona sigara tatu 'Sportsman' zikiwa zinaning'inia kwenye mfuko wa shati. Nikanehea na kutumbukiza vidole vyangu viwili nikaibana sigara kwenye pacha ya vidole vyangu na kuitoa. Nilimshangaza sana na huwenda alijiuliza kuhusiana na mteja mimi. Sikujali, niliiwasha kwa kiberiti kile cha kasha na kuitupia njiti kwenye kibakuli kilichojaa uchafu baada ya kuikung'uta kwenye hewa na kuizima. Nilivuta moshi ndani baada ya pafu kadhaa kisha nikaibana kwenye pacha ya vidole vyangu na kumtazama M.D usoni.




"Unamfahamu kwa namna gani....? Mteja au?" Nilimuuliza huku nikiendelea kumtazama. Nikamuona akimeza funda la mate na kunitazama vizuri. Badala ya kujibu alichomoa na yeye sigara moja akaniomba moto nikajua yuko kwenye bajeti kutunza njiti za kiberiti zisiishe mapema. Nikampa akaiwasha na kuvuta pafu kadhaa akanirejeshea akasema.




"Mimi na yule kijana tumesoma shule moja, hatukuwa marafiki na hata hivyo hakumaliza shule. Sikuzijua sababu zilizomsababishia kutokumaliza. Tulikuja kurejesha urafiki wetu ambao sasa ulikuwa wa kikazi siku tulipokutana maeneo fulani mjini kabla ofisi yangu sijaihamishia hapa,"




"Mlifahamiana tena kikazi? Kwani yeye anafanya shughuli gani?" Nilimuuliza swali la mtego baada ya kujiingiza kule nitakapo.




"Ni askari huyu jamaa, tena mambo yake huyafanya kwa umakini sana. Ni mpelelezi makini mno, amewahi kunipa kazi kadhaa nimfanyie hasa za utambuzi wa picha na nimekuwa nikimfanikishia mambo mengi. Dada nimekwambia haya kwa kuwa umekuwa na wasiwasi na dada yako dhidi ya watu wabaya kama si hivyo nisinge kwambia haya. Toa shaka dada yako yuko mahali salama." Alitanabaisha waziwazi M.D. Lo! Hakujua kuwa alikuwa akinifumbua masikio. Juu ya kile nilichokuwa nikikitafuta. Niliivuta sigara yangu nikiwa na matumaini makubwa sana ya kuwa karibu na wauaji ambao kwa namna moja ama nyingine wangeweza kunifikisha nipatakapo.




"Nataka kuona hiyo picha, ni ya mteja uliyesema ataifuata muda mfupi au ni ya huyu mpelelezi aliyekuja na dada yangu? Huwenda ikanishawishi nami kuchorwa." Nilimuuliza. Nikamuona akiivuta sigara yake kwa pupa kupunguza mchecheto alionao kisha akaumeza moshi wote na kutoa macho mithili ya Chatu atapikaye mifupa. Jicho likamuwiva. Nikamfananisha na Pasa ndege alaye pilipili hadi zinafikia hatua ya kumkifu. Akamagaza huku na huko utadhani anataka kunitongoza.




"Hii picha ni ya kazi dada yangu!" Hatimaye akaninong'oneza huku sura yake akiwa ameileta karibu na sura yangu, jicho lake likianza kunitisha kwa wekundu na mishipa ya damu midogomidogo iliyojitokeza kwa suruba ya kumeza moshi wa sigara na nisijue kautolea wapi maana moshi huo sikuuona ukitoka kwenye tundu nizijuazo.




Hawa ndiyo wanaounguza hadi utumbo badala ya kuunguza mapafu. Nikajiambia.




"Sawa ni picha ya kazi sikatai ni ya nani mteja au ya....!"




"Ah, ah! Dada yangu, picha hii ni ya mtu aliyemuelezea dada yako, yaani mtu anayeaminika kuwa ndiye muuaji kwa mujibu wa maelezo aliyoyatoa dada yako." Akaninong'oneza tena, ukawa ni mwendo wa kunong'onezana mithili ya watu wanaotongozana kwenye baa za mafichoni.




"Naweza kuiona?" Nikamuomba. Akacheka cheko kubwa huku akiivuta ile sigara kisha akaipiga nyundo, nikajua huwenda hata kumchukulia sigara yake kwenye mfuko wa shati nilimkera ila hakuwa muwazi. Ni miongoni mwa watu wagumu niliyowahi kukutana nao kwenye kazi yangu ya upelelezi.




Du! Hata sigara ya shilingi mia moja inapigwa nyundo? Anaweza kumhonga mwanamke kweli huyu? Niliwaza.




"Kuona....? Yaani unataka uone....? Huwa hatuoneshi vitu muhimu na hatari kama hivi maana unaweza kuona na ukaniachia, madhara yakarudi kwangu baada ya huko uendako," akaweka koma na kutulia. Akajiegamiza kitini na kunitazama akisema.




"Unalipa pesa kisha unapewa picha unatembea." Nilitabasamu na kumtazama nikamuona jinsi anavyonitazama kwa matamanio ya kutaka nikubali.






Du! Hata sigara ya shilingi mia moja inapigwa nyundo? Anaweza kumhonga mwanamke kweli huyu? Niliwaza.




"Kuona....? Yaani unataka uone....? Huwa hatuoneshi vitu muhimu na hatari kama hivi maana unaweza kuona na ukaniachia, madhara yakarudi kwangu baada ya huko uendako," akaweka koma na kutulia. Akajiegamiza kitini na kunitazama akisema.




"Unalipa pesa kisha unapewa picha unatembea." Nilitabasamu na kumtazama nikamuona jinsi anavyonitazama kwa matamanio ya kutaka nikubali.




"Pesa kiasi gani?"




"Shilingi laki moja na nusu?" Akasema. Nikaingiza mkono kwenye begi langu la kuning'iniza begani na kutoa kitita cha shilingi laki moja na kukitua mezani.




"Shilingi laki moja, nusu sina unasemaje?" Niliongea nikimtazama usoni. Nikamuona akimemesa midomo yake myeusi kama Kwembe.




"Kwanini usiongezeongeze hata ishirini dada hii ni kazi ya hatari ujue halafu nakufanyia wewe tu mwengine nisingethubutu," alichombeza katika namna ya kuhitaji nyongeza. Nikaufunga kabisa mkoba wangu nikimwambia sina. Akazichukua na kuzitia kwenye mtoto wa dawati lake na kutoka na ile picha ambayo ilichorwa kwenye karatasi ngumu. Akanikabidhi nikaitazama na kugundua kuwa ilikuwa yenyewe ile niliyoiona wakati anaificha nikaitumbukiza kwenye mkoba wangu na kusimama.




"Asante sana kaka kwa msaada wako." Nilimwambia. Nikamuona akinitazama kwa jicho kali jekundu.




"Tusijuane mimi na wewe na wazo la kuwa ulifika hapa lifute sipendi kesi dada yangu...!"




"Je, kama nikihitaji kuchorwa picha moja ya pekee sana na wewe pia nisije?" Nilimuuza nikiwa nimepiga hatua moja kama nitakaye kutoka kisha nikajiweka kimikogo na kugeuka kirembo zaidi nikiwa nimekibinua kiuno changu kilichobeba nyama laini zilizojaa kwa wastani chini yake.




"Naam!" Nilimsikia akigutuka. Nikacheka huku nikitoka na kumwambia sijawahi kuwa mtoto mdogo nisiyejua hatari wala zani.




____________




"Huu ni mwanzo mzuri sana kwangu na utanisaidia kwa kiwango nikitakacho," nilijisemea nikiwa nimekaribia mahali ambapo niliitelekeza gari yangu kwa muda. Nilitazama mazingira ya mahali lilipo gari langu, yalikuwa tulivu na hayakuleta shaka hivyo sikuwa na wasiwasi nililisogelea na kujiweka ndani yake. Nilitulia kwa muda kidogo baada ya kujifungia ndani ya gari, baada ya kujipa utulivu nikaitoa ile picha na kuitazama kwa umakini zaidi. Nilitulia nikiitazama kwa kitambo kingi loh! Niligundua kitu kwenye hii picha, sura ya huyu mtu ni kama niliwahi kuiona lakini sikuwa nikikumbuka vizuri. Nilijaribu kujikumbusha ni wapi niliiona sura hiyo hata hivyo kumbukumbu zikakataa, nikaamua kuachana na kuwaza juu ya hicho nikawasha gari na kuondoka huku nikiwa na wazo la kuelekea msibani.




Ni lazima nilale matanga. Niliwaza. Nikiwa naendesha, kumbukumbu kadhaa zilijijenga zenyewe kichwani mwangu hapa ndipo nikakumbuka ni wapi nilipata kuiona sura ya mtu pichani. Kumbukumbu zangu ziliniambia kuwa ni maeneo ya mjini sokoni. Ni mara tu baada ya kufika eneo la tukio niliiona sura ya mtu huyu akichungulia dirishani kwenye gari ile Toyota Vitara. Sikuwa na uhakika sawasawa kwani wakati namuona mtu huyo nilikuwa siko kwenye usawa wa akili na kichwa changu kilikuwa kikimuwaza mtu aliyepigwa risasi hata hivyo mtu yule alikuwa amevaa miwani ya jua na huyu pichani hakuwa amevaa miwani. Nilipofika hapo kumbukumbu nyingine zikanijia baada ya kukumbuka zile picha nilizozipiga mjini nikiwa nimeegesha gari langu pembeni ya mgahawa, alikuwa huyu na wenzake wawili. Hapa sasa nilimtambua vizuri kupitia zile picha ingawa hazikuwa kwenye ubora hata hivyo nilimhusisha moja kwa moja kwenye mauaji ya Masuka kwa kuwa siku niliyomuona alikuwa akienda kukamilisha kifo cha yule mwanausalama kikongwe.


Huu ulikuwa ni utata.




Nilikuwa tayari nakaribia eneo la tukio yaani msibani. Nilipotaka kukunja kona kuingia msibani, kuna wazo likapita kichwani mwangu nalo likaambatana na njaa. Wazo hili lilikuwa ni kuhusiana na gari. Nilifika na gari msibani na pia sikutoka garini hadi nilipowaona wale watu wawili yule kijana na yule mama wakitoka ndani na kuingia garini kisha kuambatana nao. Wazo langu ni kwamba kama kungekuwa na mtu makini ni wazi kwamba huwenda angelitilia mashaka gari langu, yumkini nilikuwa sahihi juu ya wazo langu hivyo sikulipinga. Nilinyoosha barabara na kuongeza kasi ya gari langu. Muda mfupi baadaye nilikuwa mjini nikaegesha gari pembeni na kuelekea kwenye mgahawa wa hapo mjini nikaagiza chakula kizito hata hivyo nikaomba na chai ya rangi kwani sikuwa nikilielewa tumbo langu kwani sikuwa nimetia kitu chochote tangu mawio ya jua, yumkini ningeibua mambo ambayo si ya lazima. Nilikula nikamaliza, nikalipa na kuondoka. Nikielekea mahali ninapoishi nikiwa na lengo la kuacha gari yangu kisha nirudi msibani baada ya kujimwagia maji kwani nilikuwa na hakika kuwa msiba ungefanyikia pale hadi kwisha.




__________




Ukumbi mdogo ulifurika, si watu wengi sana hata hivyo walijaa kwenye nafasi zao vile ilivyotakiwa kuwa. Watu hawa walikuwapo wengi weupe yaani watu wa bara geni, wazungu kwa lugha zoelefu. Watu wa namna hiyo walipata kuwa sita. Wawili wa kike na wane wa kiume. Wengine watatu walikuwa ni watu weusi ambao wote kwa pamoja walinawirika kwa kuridhishwa na hali ya maisha waliyonayo. Mmoja kati ya hawa alikuwa ni yule bwana mwenye kupenda kuvaa suti za rangi ya kijivu Amsuni Bhehe na wawili wakiwa ni wageni kabisa. Walikaa kama waliyokuwa wakisubiri jambo. Kimya kilikuwa kikuu hata hivyo hakikudumu sana, akaibuka Tally Man akiwa anasukuma machela yake kama ada ambayo juu yake ilikuwa imembeba mtu. Kijana huyu naye alikuwa ni mtu mweupe na hata anayemsukuma akiwa juu ya machela pia ni mtu mweupe vivo hovyo. Kwa ufupi ni kwamba watu weupe ndiyo waliyokuwa wametawala hiki kiukumbi kidogo kuliko watu weusi. Tally Man alifika hadi pembezoni mwa ukumbi ule akasimama na kugusa vitufe kadhaa kwenye ile machela kama awali na kuifanya ile machela kubadilika na kuwa mithili ya kiti cha uvivu. Malfrey Kobra akawa kama aliyekaa kwenye kiti cha uvivu macho yake yakizunguka kama Mamba. Alitabasamu baada ya kuwaona watu aliotegemea kukutana nao mahala hapo kisha akatikisa kichwa juu chini kwa kuridhishwa kabisa.




"Umefika muda gani kutokea Uganda Mr. Polgeo?" Aliuliza Malfrey akiwa anamtazama mzee mmoja wa kizungu ambaye alikuwa na nywele nyeupe kichwa kizima, zilizokatwa kwa usawa akiwa amevaa miwani ya macho. Alikuwa mfupi mwenye kitambi cha wastani akiwa amevaa shati jeupe. Alitabasamu yule mzee kisha akamtazama amuulizaye.




"Ni masaa machache tu na nimetumia usafiri wa familia ambao nauamini pia rubani wangu yuko makini mno, niko na vijana wangu na binti yangu. Hii ni ishara tosha kuwa nimekuja kamili na sibanduki hadi kieleweke." Akasema Mr. Polgeo akiwa na furaha isiyo kifani.




"Nawaona vijana wako, namuona binti yako Miss Anna hata hivyo namuona Mrs. Polgeo akiwa kwenye ubora wake." Akaongea Malfrey akichomekea na kautani ndani yake.




"Hakika Malfrey. Nipe mpango ulivyo? Unajua tunachokifanya ni kitu kikubwa sana na kimefanikiwa kwa kiasi kikubwa mno. Nafikiri kwa kina hapa kama angelikuwapo Maleley Kobra sijui ingekuwaje. Nchi hii ingeimba 'Haleluya'. Sifikirii mimi nchi kama hii isiyo na hiatoria mbaya ya hatari ifanye mambo ambayo hata nchi zinazosifika haifanyi. Hatuwezi kuwa kwenye mashaka tena Malfrey, huyu Rais mpuuzi nampa siku chache lazima abadili wazo lake la kutuachia sisi wawekezaji tufanye tuyatakayo. Migodi yote inayomiliki madini mengi kama Dhahabu, Almasi na Uraniam, kwanini waweke vikwazo na kudai tulipane nusu kwa nusu. Wanajua ni kwa namna gani tunatumia gharama kuchimba madini? Sawa bado ni faida kubwa tulikuwa tunavuna pamoja na huko kuhitaji tugawane nusu kwa nusu, mpuuzi huyu Rais amezuia hadi sisi kusafirisha mchanga kwenda nje akidai ni madini mengi yanaibwa kupitia ule mchanga? Ile ndiyo ilikuwa faida yetu kubwa na tulikuwa tukichuma pale. Hapa ndipo nilipochanganyikiwa Malfrey na hapa ndipo walipoutibua ugonjwa wa Maleley na kupelekea kifo chake na walipoifunga loh! Wakammaliza kabisa. Nimekuja kusimama kama Maleley Kobra....nimekuja kama mzimu. Nimekuja na mbinu kubwa za kutisha ambazo zitasababisha huyu Rais akubali kurudisha moyo nyuma hata kama ni kwa siri bila wanachi kujua ili sisi tuendelee kuvuna mali, tangu lini nchi ya watu wajinga, watu wasiyojua kusoma hata maandishi ya mkataba, watu wasiyojua kujitengenezea mavazi ya kusitiri tupu zao wenyewe, watu wanaojua kupokea misaada bila kujua kwenye hiyo misaada kuna madeni tumewapandikizia, watu ambao ubongo wao umejaa giza kama bara lao lilivyo na giza, watu wapuuzi, watu waishio kwenye bara linalonuka umasikini wakati utajiri wanao, iweje....nasema iweje watuwekee vikwazo vya kutuzuia sisi tusivune. Nilichokuja nacho ni hiki; lazima tuzuie dawa za magonjwa muhimu zisiingie nchi mwao....ndiyo, na nimefanya hivi kwa makusudi makubwa sana, tusipokuwa makini na kuwa na roho mbaya wanaweza kututafutia hata wanaume wa kutuoa wapuuzi hawa!" Aliongea kwa uchungu mkubwa Mr. Polgeo.




"Fuck you Mr. Polgeo....Hah hah hahaaa! Kwanini sikuwa nimewaza hivi? Kwanini kichwa changu kilijaa kunguni waliokuwa wakiufyonza ubongo wangu na kujipasukia wenyewe huku wakiniachia harufu mbaya ya damu yao iliyokuwa ikiniumiza pua zangu. Hakika mtu mweupe milele atabaki kuwa wa thamani, mtu mweusi ni kitu gani bwana!" Alitamba Malfrey huku akiunyanyua mkono wake mmoja akiwa amekunja ngumi. Amsuni Bhehe alijihisi vibaya mno mbele ya watu hao, alijiona kama mtoto avuliwaye nguo na shangazi yake kisha akatusiwa 'muone kifilimbi chake kama cha baba yake wakati mdogo nikimuogesha'.




Hii ilikuwa ni fedheha kubwa. Angefanya nini wakati pesa ilikuwa inanguvu kuliko maneno ya kashifa anayotukanwa. Pesa, pesa...ndiyo, pesa ilikuwa ikimchambisha anapojisaidi, kumnawisha wakati wa kula na kumlisha vile atakavyo. Pesa kwake ilikuwa ni zaidi ya matusi hivyo hata angetukaniwa mama yake mzazi aliye malaloni kwa miongo mitatu iliyokwisha kukatika akiwa kwenye nyumba yake ya milele bado angekenua tabasamu kama hayawani.




Ujinga.




Hii ilikuwa inatafsirika kabisa kuwa Afrika ilinuka umasikini na ilhali utajiri ulikaliwa nao. Akajivika ujeuri wa maji kwenye kinu, hata uyatwange hayabadili umbo.






Pesa kwake ilikuwa ni zaidi ya matusi hivyo hata angetukaniwa mama yake mzazi aliye malaloni kwa miongo mitatu iliyokwisha kukatika akiwa kwenye nyumba yake ya milele bado angekenua tabasamu kama hayawani.




Ujinga.




Hii ilikuwa inatafsirika kabisa kuwa Afrika ilinuka umasikini na ilhali utajiri ulikaliwa nao. Akajivika ujeuri wa maji kwenye kinu, hata uyatwange hayabadili umbo.




Semeni lakini changu kinywani. Akajisemea moyoni huku sura yake pana ikimshuka kama soksi ya hayawani mtembea hovyo. Akakubali yote kibwege tu Amsuni.




"Tunaupa jina gani huu mpango?" Akauliza Malfrey baada ya kutoka kushangaa kama ada yake afikwapo na mshangao usiozuilika kutokana na ugonjwa wa saratani ulioanza kuathiri ubongo wake kwa uchache sana huku jitihada za kumfanya aishi zikiwa juu kwa kiwango kikubwa na hayo ndiyo maisha yake ya kuishi katika tiba hadi kifo chake.




"Mpango wa nje na nina uhakika kabisa Malfrey kuwa mpango huu litakuwa ni pigo butu la kifo. Hawatajua ni nani amezua hili balaa, watakufa sana kwenye mpango huu mbaya, watakufa huku anayewaua wakiwa hawamjui. Hebu fikiria tukizuia dawa za kusogeza siku kwa wagonjwa wa ukimwi, dawa za kifua kikuu, dawa za ugonjwa wa sukari na shinikizo la damu, dawa zinazosaidia huduma ya saratani mbalimbali na kadhalika. Rais hata kubali kuruhusu kila kitu kiwe chetu...? Umeona utamu huo. Hata hivyo wakiomba msaada kwenye mashirika ya afya watapindishwapindishwa au kupewa dawa zisizotosheleza halafu zikija bado zitaishia kwenye makwapa yetu hadi watie akili na mkuu wa nchi asalimu amri na hili litawagharimu kwa kiasi kikubwa mno. Baada ya mwezi mmoja baada ya zuio hilo ndipo tunapigilia msumari wa moto kwa Rais Ikulu kuwa tunahitaji mkataba wa sheria mpya ya madini ule waliouunda wao wa nusu kwa nusu ubadilishwe. Hatuwezi kukubaliana na vikwazo walivyotuwekea kiasi kwamba tunashindwa kufanya biashara zetu hata hivyo hatuwezi kuiachia hii migodi na wengine wachukue wakati sisi ndiyo wamiliki. Wafute vikwazo walivyoweka vya kipumbavu ambavyo vimegharimu maisha ya viongozi wao wapumbavu wale. Muheshimiwa Rais akiwa jeuri basi; tunamwambia taifa litakushangaa kama utaendelea kuwaacha raia wake wafe kisa mali ambazo kwazo kuna chochote kitu kitaingia pia huku wakiwa hawapati madhara?" Akahitimisha Mr. Polgeo kisha akavuta bilauri ya maji akagida na kuishusha mezani ikiwa na maji robo tatu.




"Natumai mpango huu hautaleta madhara kama ule uliotokea mwanzoni, mpango huu utaniondolea au kunipunguzia machungu ya ndugu yangu. Naumia sana Mr. Polgeo ninapokaa na kumkumbuka ndugu yangu, kuna muda huwa machozi yananitoka kabisa. Maleley aliwakosea nini? Aliwakosea nini Maleley ndani ya taifa hili? Ni baada ya kuidai haki yake mahakamani, hawakujua kuwa alichokuwa akikipigania ni hasara aliyoipata kwa kuzuiwa asiendelee na uchimbaji kwa kisingizio kuwa alikuwa hajali maisha ya raia. Kwanini walimsimamisha na wasimwambie aweke sawa mazingira. Watalipa, watali.....!" Alishindwa kumalizia Malfrey machozi mazito yakamtoka, akayafuta na kukumbuka miaka mingi iliyokwisha kupita huko nyuma.




_________




MIAKA 20 ILIYOPITA.


VICHEKO VILIKUWA VIKIRINDIMA NDANI YA JUMBA MOJA KUBWA HUKO KWENYE JIJI LA SAMI ADO, furaha ilidhihirika ndani ya jumba hilo na ilionesha wazi walioko ndani hawakuwa na mawazo haya ya kimaisha kama wengine wawazavyo na kama yalikuwepo basi yalitofautiana. Vicheko hivyo kamwe havikukoma kwa haraka na nyuma ya hivyo vicheko kulikuwa na soga ambazo zilikuwa zikiendelea.




Yalikuwa bado ni majira ya mchana, kajua kalikuwa kakali kimtindo lakini kasichowazuia watu kuendelea na pilika zao zile walizozizoea kila siku. Lilikuwa ni jumba kubwa ambalo lilibeba ghorofa moja, mandhari yake ya nje ilivutia kwa maua yaliyopandwa kistadi na mitimiti mingi iliyoweza kuweka kivuli. Haikuwa na uzio wa aina yoyote bali ilikuwa na mlango mgumu wa chumba uliyotangulia kabla ya mlango mwengine wa mbao ngumu kufuatia. Korido yake ilikuwa pana na ndefu kama ungebahatika kuingia ndani ya korido hiyo na korido hiyo ndiyo iliyokuwa ikimfikisha mtu anayetokea mlango mkubwa wa mbele hadi kwenye sebule hiyo kisha ndiyo huamua kukwea ngazi ambazo humpeleka kwenye ghorofa ya kwanza ama jengo la juu. Kwenye korido hii kulikuwapo na watu watatu ambao hasa ndiwo waliyokuwa wakipiga soga na kuangua vicheko vikubwa vya kuridhishwa na maisha waishio, maisha ambayo hayakuwa yakiwafanya wahisi kitu kinachoitwa ukata kama kipo kwenye koo zao. Miongoni mwa hao watu watatu walikuwapo mapacha wawili Maleley Kobra na Malfrey Kobra ambao ndiwo wamiliki wa jumba hilo kubwa. Maleley alikuwa ni mmiliki wa kampuni kubwa za uchimbaji wa madini zipatazo tatu. Kampuni moja ilikuwa ikihusika na uchimbaji wa madini aina ya Almasi ambayo ilikuwa Haika. Hii ilikuwa ni kampuni aliyokuwa akiitegemea sana ambayo iliitwa Maleley Unity Mining Company (M.U.M.C). Kampuni nyingine ya pili na ya tatu hizi zilikuwa kwenye jiji la Sami Ado, pembezoni kabisa mwa jiji hilo ambalo hata wao wenyewe waliamua kuweka makazi humo. Moja ilikuwa ikijihusisha na uchimbaji wa Dhahabu, hii ilikuwa ni moja ya kampuni kati ya mbili za kushirikiana na ndugu yake na zote zilibeba jina la M. Ambapo huu uliitwa M.U.M.C ikiwa na maana moja tu kama ile ya awali. Huku mgodi wa tatu ambao ulikuwa mkubwa zaidi ambao ulikuwa ni mgodi mama kama ule wa Haika, ukiwa ni mgodi pekee unaowaingizia pesa nyingi, mgodi huu ulijihusisha na uchimbaji wa Uranium ambao ulimilikiwa na Maleley akiwapo na huyo mzungu mzee anayefahamika kwa jina la Mr. Polgeo. Waliupa jina la S.A.M.C. Ikiwa na maana Sami Ado Mining Company. Migodi hii iliwapa utajiri mkubwa sana na iliwaweka kwenye ramani ya wawekezaji ambao walikuwa wakimiliki utajiri mkubwa kutoka Bara la Afrika. Huyu mwingine wa tatu alikuwa ni mtu makini na anayemuamini sana bwana Maleley huyu alimuamini kwa kila kitu hususan ulinzi wake na alikuwa bado ni kijana mdogo sana ukimuangalia hata hivyo alikuwa na uwezo mkubwa wa kuutumia mwili wake katika tasnia ya mapigano ya kujilinda kwa kutumia mwili na mapigano ya kujilinda kwa kutumia silaha. Aliitwa Tally Man. Alikuwa mdogo mno kiumbo na umri kijana ambaye ukimtazama kwa woga unaweza kudhani ni kiziwi au bubu maana si mara kwa mara hupenda kuongea.




Sebuleni hapo kulikuwa na runinga kubwa ambayo ilikuwa ikionesha burudani ya muziki laini huku waimbaji wake wakiwa wamevaa nguo za nusu utupu. Midomoni mwao kulijaa Tambuu ambazo walikuwa wakizitafuna kwa sifa kubwa watu hao.




"Nina mpango wa kwenda Uingereza siku za usoni Malfrey." Aliongea Maleley pacha wa Malfrey. Malfrey akamtazama nduguye, Tambuu na pombe kali vilikuwa vimekwisha kuanza kumchukua tayari.




"Uingereza?...Uingereza kufanya nini? Au ndiyo unamfuata yule malaya anayekupa nyama adimu yenye mafuta kama nyama ya Bata mzinga?" Akaongea Malfrey kwa kuuliza huku akionekana kukosa nguvu ya macho yake kutokana na kuzidiwa na kilevi.




"Kuna mzigo unatakiwa kwenda London, ambao ulishalipiwa tayari hata hivyo nimemkumbuka sana Mary, nimekumbuka nyama yake ya nyuma anayo nipa, kama unijuavyo kuwa sili mahali pengine zaidi ya kule, Afrika wapo wanawake wazuri na wenye utamu wa kuzichanganya akili za watu hata hivyo hawaufikii utamu wa Mary na nimemkumbuka sana." Akazungumza uharamu wake Maleley huku akizidi kuibugia pombe, soga zikanoga na vicheko kuongezeka. Kijana Tally Man raia wa Urusi alikuwa kimya akiwatazama ndugu hao walivyokuwa wakiyafurahia maisha.




"Wanawake wapo kwa ajili yetu na wameumbwa ili tuwatumie, tunawala kila sehemu ambayo tunajisikia kula na kwa kuwa wao wapo kwa ajili yetu, wanasikia raha tunapo watafuna....yuhuuuuu...! Wacha tuinjoy maisha 'my brother," akaweka koma Maleley Kobra kisha akasimama na kuyumba kidogo akatazama runingani ambako kulikuwa na mwanamke aliyekuwa amekaa pembeni ya Jakuzi akiimba huku akijishika mapaja yake na kuchezea kifua chake kilichobeba matiti mazuri.




"Tazama malaya, tazama mtoto mweupe wa kike wanavyovutia, tazama walivyonona, unadhani Afrika kuna Nyani wa kufikia pale. Watu weupe ni daraja la juu bwana huku kuna warembo basi zaidi ya kujimalizia haja zetu tu." Akamalizia huku akiondoka kwa mwendo wa kuyumbayumba na kuelekea msalani kwenda kupunguza maji yaliyojaa kwenye kibofu chake, haja ndogo ilimbana hasa.




"Kaka anapenda starehe na maisha yake yote yeye analawiti tu, hajawahi kufanya mapenzi kwa njia ya halali na huwa hachagui anaweza kusema amemkumbuka Mary kumbe anakwenda kula raha na mashoga ya huko Uingereza. Very dangerous man my brother." Akasema Malfrey huku akichukua rimoti akabadilisha idhaa. Ilikuwa ni taarifa ya habari iliyokuwa ikirushwa na kituo kikubwa cha nchini hapo.




"Kwanini unatoa wakati tunataka kuangalia malaya wanavyojishikashika?" Alifoka Maleley Kobra akiwa anafunga zipu ya suruali yake akiwa amesimama hatua mbili nyuma ya Malfrey baada ya kutoka msalani.




"Tunarudisha sasa hivi kaka ngoja tuangalie wanasemaje hawa wajinga maana.....!"




"Mgodi mkubwa wa Almasi ulioko Haika pembezoni mwa misitu ya Gonja wafungwa rasmi....!" Taarifa hii ilimfanya Malfrey ashindwe kumalizia kauli yake na kuiacha ikiogelea hewa. Vichwa vyao wote watatu vilianza kuvurugika. Taarifa ile iliendelea.




".....Waziri wa nishati na madini muheshimiwa Tadeus Mkwayu akiambatana na waziri wa Afya muheshimiwa Bi. Rukia Salmini, wafanya ukaguzi wa kushtukiza kwenye kampuni hiyo kubwa ya uchimbaji wa madini hayo ya Almasi yenye thamani kubwa na kugundua mambo mengi ya hatari yenye kuhararisha afya za wafanyakazi pamoja na wananchi waishio karibu na mgodi huo. Muheshimiwa Rukia Salmini ndiye aliyesimama kidete na kutoa tamko kali dhidi ya mgodi huo. Kwanza kabla ya tamko hilo kutolewa alitafutwa mkurugenzi mkuu wa mgodi huo ili aweze kujibu shutuma hizo za kuwafanyisha watu kazi katika mazingira hatarishi hata hivyo zoezi la kumtafuta mkurugenzi huyo liligonga ukuta. Mwamama huyo hakusubiri jua lizame maana si mara moja wala mara mbili walishawapa angalizo wamiliki wa mgodi huo hata hivyo wakapuuza na kudharau. Muheshimiwa Rukia akasema kuwa kuanzia muda huo mgodi huo ufungwe na usiruhusiwe kufanya kazi zake hadi pale watakaporidhishwa na hali ya mazingira yaliyomo ndani ya mgodi na yale yanayouzunguuka mgodi huo." Taarifa hii ilikuwa ni mwiba kwa ndugu hawa, kila mmoja alichanganyikiwa na hakujua afanye nini kwenye hili. Ni kweli simu zao zote wawili hazikuwa zikipatika, walizima simu zao ili wasiweze kubughudhiwa na mtu yeyote wakiwa kwenye starehe zao kumbe kilichokuwa kikienda kutokea ni kibaya kuliko walivyodhani. Maleley akaomba Mungu isiwe kweli, akawasha simu. Ikawa kama alikuwa akisubiriwa afanye hivyo ili simu ziweze kuingia.








Ni kweli simu zao zote wawili hazikuwa zikipatika, walizima simu zao ili wasiweze kubughudhiwa na mtu yeyote wakiwa kwenye starehe zao kumbe kilichokuwa kikienda kutokea ni kibaya kuliko walivyodhani. Maleley akaomba Mungu isiwe kweli, akawasha simu. Ikawa kama alikuwa akisubiriwa afanye hivyo ili simu ziweze kuingia. Simu zilipigwa kwa wingi kama mvua kutoka kwa watu mbalimbali kama wafanyakazi wao na kadhalika na walipopokea Maleley aliganda kwa sekunde kadhaa kabla ya kupata uhai wa kuongea. Akaondoka hapo hadi kwenye kampuni zake akitumia usafiri wa chopa. Alipofika huko alikutana na wafanyakazi wakiwa wamejazana kila mmoja akisema lake. Akapata maelekezo na maelezo yote kutoka kwa meneja uzalishaji kwani yeye ndiye aliyekutwa pekee eneo la kazi.




"Hili unatakiwa ulifuatilie kwenye wizara husika bosi," alitoa ushauri Meneja huyo akiongea kinyonge kwani hakuwa na uhakika kama angeweza kupata kibarua karibuni ambacho kingekidhi mahitaji yake. Maleley Kobra hakusubiri alichukua gari na kuelekea mahali alipoelekezwa. Alifika kwenye ofisi hizo za kiserikali akakaribishwa hata hivyo alichokutana nacho ni kwamba kilimfanya ajihisi mapigo ya moyo wake yakienda mbio na kukosa pumzi kwa wakati. Migodi yake yote ilikoma kulipa kodi karibia miaka nane iliyopita. Akajihisi kuumwa kwa kukumbwa na shutuma hizi zenye ukweli aliokuwa ameuficha kibindoni.




Hili lilikuwa kweli lakini ipo misingi au sababu za kufanya hivyo naye kama mkubwa wa tuhuma hizo za kutokulipa kodi. Akatakiwa kutoa sababu za kutokulipa kodi kwa miaka yote hiyo huku akilisabishia taifa hasara. Akatoa sababu zake alizoziona ni za msingi hata hivyo hakuwa na umahiri wa kuzitolea hoja ya kutosha kwani hata sura yake ilimpwaya, pombe zikamchanguka ghafula na kujiona anapoteza kila kitu. Akaomba radhi kuwa mchakato wa kulipa utafanyika kwa haraka na kwa kasi ya ajabu hata hivyo hoja zake hazikuonekana ni sababu za kushiba hivyo hata maombi yake hayakupewa mashiko. Maamuzi magumu yalishapita na hakukuwa na mjadala wowote hivyo kwa shutuma hizo na kukiri kwake migodi yote ikafungwa.


Akagonga mwamba Malfrey.




Akajaribu kufuatilia huku na kule hata hivyo hakufua dafu. Miaka sita ikakatika akiwa bado anafuatilia haki zake za msingi kama kukubali kufanya au kuweka mazingira katika hali ya usafi na kuwafidia wale wafanyakazi wote waliofutwa kazi kwenye kampuni zake kwa kupata maradhi yatokanayo na shughuli za uendeshwaji mbaya wa migodi yao, waliopata vilema na kadhalika huku akilikwepa kosa la ulipaji kodi kwa muda huo wa miaka nane mizima akijifanya hamnazo. Nani wa kukubali upuuzi huo na ilhali alishashikiwa bango si chini ya mara moja kuwa kulipa kodi kwa makampuni yote ni wajibu? Yeye au wao ni akina nani hadi waogopwe? Hakuna mpuuzi wa hivyo...hakuna. Rais aliyekuwa madarakani kwa kipindi hicho muheshimiwa Ngao Kambi akatoka kwenye kiti hicho cha u-Rais mabwana hao wakiwa hawajatekeleza lolote huku kimya wakikiona kama ni sehemu ya matekelezo yao. Muheshimiwa Kambi alikwenda kumkabidhi kiti hicho cha u-Urais muheshimiwa Mobande Julio Mobande. Huyu akabadili kila kitu kwenye wizara mbalimbali na kupanga kila kitu upya, akasababisha mvurugano mkubwa sana. Na kwenye mgodi ule akahitaji muwekezaji mwengine huku wale wa awali akiwa hawatambui tena kwani muda wa makubaliano wa kimkataba ulishapita.




Hatari ikaanzia hapa.


Hapa walimchafua Maleley Kobra. Akaleta mawakili na wanasheria waliobobea lakini wanasema mwenye chake ana chake. Maleley Kobra akaambulia hasara iliyompa ugonjwa wa kuanza kupoteza fahamu mara kwa mara hatimaye akawa mtu wa kukakamaa mithili ya mgonjwa wa kifafa. Maleley Kobra akawa mtu wa kitandani baada ya afya yake kuwa mbaya zaidi maana hakuwa sawa na muda mwingine alikuwa kama mtu aliyechanganyikiwa kiakili. Ulikuwa ni ugonjwa usioleweka kabisa. Hali hii ikamdhoofisha hata Malfrey. Wakaomba msaada nje kwa ajili ya kusaidiwa hili lakini Maleley mwenyewe akagoma akasema hahitaji msaada kutoka nje ya nchi, aliona ni fedheha kubwa mno kuzidiwa akili na wapuuzi ambao hawana uwezo hata wa kutengeneza kidonge cha kumuangamiza Mbu, pia akasema hahitaji kutibiwa nje ya nchi na hahitaji daktari wa nje bali anahitaji daktari kutokea Afrika au Afrika ya mashariki ambaye atahakikisha anaisimamia afya yake hadi itakapotengemaa aweze kusismama ndipo apange mipango ya kulipa kisasi au kurudi tena mahakamani kwa kishindo. Kutafuta madaktari nje huku sababu ya ugonjwa wake ikiwa ni ile kuzidiwa akili na watu wenye ngozi nyeusi.




Hakutaka. Alitaka Afrika yenyewe ndiyo impatie madaktari wenye kuweza kumsaidia na si vinginevyo, asingependa fedheha ile ikawa ni mbinu ya kumuharibia.


Hapa ndipo palipoibuka kazi ngumu ambayo Malfrey hakuwahi kuifikiria. Kutafuta madaktari bingwa Afrika? Ilikuwa ni kazi ngumu ambayo hakudhani kama angefanikiwa kwani hakuamini kama ndani ya Afrika tena Afrika ya mashariki kungekuwa na madaktari wa aina anayoitaka.




Ilichukuwa muda na afya ya kaka yake, pacha wake ikizidi kuzorota. Maleley alikuwa na uwezo wa kupoteza fahamu kwa muda wa masaa sabiini na mbili bila kuzinduka. Malfrey akatafuta watu makini kutokea kwenye nchi tatu, watu hawa walikuwa ni viongozi ndani ya nchi hizo, nchi hizo ilikuwa Tanzania, Kenya na Uganda. Pesa kubwa ililipwa kwa ajili ya kazi hiyo na hawa watu ambao walikubali kuuingia mkenge huo walikuwa ni mawaziri wa afya ndani ya nchi hizo. Hii ilikuwa ni kazi rahisi sana. Muda wa juma moja tangu kutolewa kwa kazi hiyo. Kulikuja majina mengi kutoka kwenye nchi hizo za madaktari bingwa na sifa zao. Malfrey akapenda madaktari wawili tu kutokea Tanzania ambao walikuwa na sifa mbili tofauti. Alikuwapo Daktari bigwa wa magonjwa ya saratani pia alikuwapo Daktari bingwa wa magonjwa ya akili na mchunguzi wa magonjwa yafananayo na hayo. Kilichomvutia Malfrey ni sifa za madaktri hao, sifa zao zilishiba katika utoshelevu wa kuaminika. Baada ya kuridhishwa na sifa za madaktari hao, ukaja mpango mwingine wa namna ya kuwapata maana jambo hilo lilitakiwa kuwa siri kubwa pasipo mtu yeyote kujua kama madaktari hao wapo wapi na kwa misingi ipi. Ile kauli ya kumhadaa mtu mweusi kwa pesa ni rahisi ikatumika kikamilifu. Mpango huu ukaundwa kwa haraka sana, wakatafutwa watu wenye akili ya kazi ambao walikuwa wanajua nini wafanyacho na kwa wakati gani na ndani ya mpango huo alikuwapo kijana mdogo kipindi hicho Tally Man akiwa na vijana wengine wawili. Hawa wakatumwa nchini Tanzania, wakaenda kusoma mazingira na namna ya kujua ni kwa namna gani wataweza kuwakwapua wataalamu hao eidha kwa hiyari yao ama kwa shuruti.




__________




Ni siku hii asubuhi na mapema kabisa huko Tanzania mkoani Morogoro, Dokta Lumoso Papi Mmbai alipokuwa akitokea nyumbani akielekea kazini kwake. Hakuwa akijua kitu kwamba ni siku ya tatu imetimia tangu kuwa na mtu aliyekuwa akimfuatilia na kumtaka afanye atakavyo pasipo kumuelewa. Siku hii alifika hospitali na kufanya shughuli zake kama ratiba yake ya kazi ilivyomtaka awe. Alikuwa akionekana kuwa na mambo mengi sana akilini yaliyomnyima utulivu, hii ikampelekea kuwa kama Mbayuwayu maana hakuwa na kituo cha muda mrefu mahali pamoja alielea na sakafu ya kutokea ofisini hadi wodini, wodini hadi maabara kisha kurudi ofisini tena. Wakati safari hizi zikiwa zinaendelea akiwa ndani ya koti lake refu la kidaktazi bwana huyo ambaye alikuwa na mwili mkubwa kidogo, kidevuni akiwa hana hata ndevu moja, kichwani alinyoa upara uliyokuwa unawaka hasa na hii hakuifanya kwa bahati mbaya la! Dokta Lumoso Papi Mmbai alibarikiwa uwaraza mbaya sana uliyotokea juu kidogo ya paji la uso hadi karibia na shingo upande wa nyuma. Alijiona bado kijana na kwa umri ule kuwa na uwaraza ni kama kiongozi wa dini na mkoba wa uchawi. Akaamua kuwa mtu wa mapara kila ahisipo visiki vya nywele kutaka kuota kwa zile sehemu chache zilizobarikiea nywele. Ilikuwa yapata saa nne na nusu sasa na hakujua kutia kitu ndani ya tumbo lake hata hivyo bado alikuwa na zaidi ya wagonjwa wawili walio katika hali mbaya sana ambao alishawafanyia vipimo huku wachache akiwapatia majibu na nini cha kufanya na wengine kati ya wachache hao akiwapa uhamisho wa kimatibabu kutoka Hospitali hiyo ya manispaa ya Morogoro kwenda kwenye Hospitali kubwa ya taifa ya Muhimbili jiji Dar es salaam kutokana wagonjwa hao kuwa katika hali isiyowezekana kwenye Hospitali hiyo. Alibakiwa na wagonjwa watatu ambao hawa hakuwa amewapatia majibu ya vipimo vyao na hiyo ni kutokana na kuwa bado hakuwa amefanya uchunguzi wa vipimo vyao. Alikuwa akirudi ofisini kwake kwa lengo la kuangusha njuga chini baada ya tumbo kumzidi hoja ya uhitaji wa chochote kitu. Taharuki kubwa inamkumba baada ya kukutana na mtu ambaye kwake alikuwa ni wa ajabu sana. Hakuwa na miadi naye, hakumhitaji kwa muda huo ambao tumbo lake lilimlaumu juu ya ucheleweshwaji wa chakula pia hakuwa mstaarabu wa ukaribishwaji kwenye ofisi za watu.




Huyu alikuwa wa tofauti alikiri.


Alitaka kurudi nyuma na kutimua mbio baada ya kugundua kumbe hata mtu mwenyewe hakuwa akimjua.




"Usikimbie, hakuna tatizo usikimbie....kuwa na amani mimi ni mhitaji wa huduma yako Dokta." Alisema yule mgeni akiwa kwenye utulivu mkubwa sana huku akiivuta sigara yake taratibu akiwa juu ya kiti cha wageni. Walau Dokta Lumoso Papi Mmbai akapata ahuweni ya moyo, mapigo yakajaribu kutafuta njia ile ya upigaji wa awali akamtazama mtu huyo kwa umakini. Akajipapasa harakaharaka kwenye mifuko ya suruali yake akatoa pakiti ya sigara iliyokunjamana na kuchomoa sigara moja ambayo kabla ya kuiweka kwenye kingo za midomo yake, aliinyoosha kidogo baada ya kuwa imejikunja kisha akatafuta kiberiti kilipo hata hivyo akashangaa kasi ambayo aliitumia yule mgeni kuwasha kiberiti cha gesi na kumsogezea moto. Pamoja na mshtuko uliyomkumba hata hivyo aliibana sigara yake vizuri kwenye kingo za midomo yake na kuuinamia moto usoni akiwa na tashwishi kubwa. Akaiwasha sigara yake huku akimtazama mtu huyo na asimmalize. Alikuwa mzungu mtu yule.




"Wewe ni nani na unahitaji nini ofisini kwangu?" Akauliza Dokta Lumoso Papi Mmbai baada ya kuvuta mapafu matatu mfululizo ya sigara yake akijaribu kuifukuza hofu moyoni mwake.




"Hukai kwenye kiti Dokta?" Yule kijana mdogo wa kizungu akauliza badala ya kujibu. Kitu kilichomuogopesha Dokta Lumoso ni kwamba kijana huyu alikuwa na asili ya Uzungu hata hivyo aliongea lugha ya Kiswahili kwa uzuri.




"Nina njaa sana na pia nina kazi kubwa ya uchunguzi ambayo natakiwa kuitolea majibu leo hii kabla ya alasiri." Akajibu Dokta Lumoso akimtaka mtu huyo aseme kilichomleta.




"Ni maongezi ambayo hayamalizi hata dakika moja Dokta, ungekaa nadhani tungeelewana zaidi." Akasihi yule mtu. Dokta Lumoso akajivuta na kukikaribia kiti cha pembeni hakukaa kwenye kiti chake cha ofisi. Yule kijana akageuka na kumtazama yeye kisha kijana huyo akaivuta sigara yake huku Dokta Lumoso naye akimfuatisha kijana yule aliyeonekana kuwa ni mwenye asili ya Kirusi akatabasamu.




"Naitwa Tally," akatabasamu tena kabla ya kuendelea.








Dokta Lumoso akajivuta na kukikaribia kiti cha pembeni hakukaa kwenye kiti chake cha ofisi. Yule kijana akageuka na kumtazama yeye kisha kijana huyo akaivuta sigara yake huku Dokta Lumoso naye akimfuatisha kijana yule aliyeonekana kuwa ni mwenye asili ya Kirusi akatabasamu.




"Naitwa Tally," akatabasamu tena kabla ya kuendelea.




"....Si mgonjwa wa akili ni jina langu, sijui ni kwanini nilipewa jina hili sijui, labda ni kwa vile nilivyo," akavuta tena sigara na kupuliza moshi juu kwa madaha akatulia. Udogo wa umbo lake na umri wake haukumtaka awe mvutaji wa sigara hata hivyo Dokta Lumoso hakujaji sana kuhusu hilo kwani huwenda ni tabia aliyoirithi kutoka kwenye koo zao.




"Nataka jambo moja Daktari....hauko peke yako uko na Daktari mwenzako bingwa kama wewe, najua mko na kazi nyingi hata hivyo ya kwangu ni muhimu zaidi. Wewe na huyo daktari mwenzako mnatofautiana ujuzi. Wacha nikuume sikio....uko na Daktari wa magonjwa ya akili, ni mjuzi sana wa matatizo ya ubongo....heh heh heee! Mnaweza kushirikiana kama inawezekana hata hivyo nataka iwe siri baina yenu nami. Dokta Omary Maboli Siki, unamfahamu....? Najua unamfahamu maana mnafanya kazi kwenye kituo kimoja...sasa sikia jambo lenyewe ni hili hapa." Akaweka tuo kisha akasimama na kuivuta tena sigara yake. Akarusha hatua mbili za upole mithili ya Kinyonga lo! Huyu bwana mdogo alizidi kumuacha njia panda Dokta Mmbai.




"Nataka ufanye uchunguzi wa ugonjwa huu ambao nitakueleza kwa uchache dalili zake za nje. Mgonjwa huyu anasumbuliwa na maumivu ya kichwa, anapoteza fahamu pengine hata siku tatu pasipo kuzinduka, anakakamaa na kulalamika maumivu ya kiuno mgongo....unaweza kufanya uchunguzi wa mgonjwa mwenye dalili hizo?" Akauliza yule Tally baada ya maelezo marefu kidogo.




"Hapana siwezi, kwa kawaida tunafanya uchunguzi baada ya vipimo kufanyika hatufanyi uchunguzi wa dhania kijana."




"Ooh! Lakini nimekueleza namna mgonjwa alivyo, si jambo la mzaha ni mgonjwa aliye katika hali mbaya sana na unahitajika msaada wako,"




"Sijawahi kufanya kazi hivyo na sitawahi kufanya kazi hivyo, nina misingi kwenye kazi hii ambayo nayo inataratibu zake kama zilivyo kazi nyingine. Mgonjwa huwa analetwa Hospitali au kama huhitaji mgonjwa wako aje hospitali zipo taratibu za kufuatwa ili mgonjwa wako aweze kutibiwa nje ya Hospitali si kihunihuni kama hivi."




"Ooh! Nimepata wazo na umenifumbua masikio. Kumbe kunauwezekano wa mgonjwa wangu kutibiwa nyumbani. Si hapa lakini ni nchini Ungamo. Ooh! Musa....! Umepona sasa najua umepona....Dokta, inabidi ufanye uchunguzi kuhusiana na dalili nilizokueleza ili mgonjwa wangu nijue anasumbuliwa na nini?" Akasema Tally akiwa amepoteza tabasamu na ile sigara kuitupia kwenye kikombe kigumu cha udongo cha takataka hizo ikiwa nusu huku ikirndelea kufuka moshi mwepesi.




"Unahitaji uchunguzi gani? Dalili ulizozitoa hapa zinaingiliana na magonjwa mengi sana naweza kusema ni ugonjwa wa Uti wa mgongo (Meningitis). Kulingana na dalili ulizosisema maana hata mgonjwa wa Uti wa mgongo hupoteza fahamu, hukakamaa mithili ya mgonjwa wa kifafa pia husumbuliwa na maumivu ya kichwa ambayo hupelekea kupatwa na kitu kiitwacho 'Phonophobia' kitaalamu, hali hii humfanya mgonjwa kushindwa kuhimili sehemu zenye kelele. Hizi zote umezitaja. Vilevile kupitia dalili ulizosisema naweza kukwambia mgonjwa wako ana Saratani ya Ubongo, Uti wa mgongo na kadhalika. Mgonjwa wa Saratani ya Ubongo pia anazo dalili hizo. Unadhani sasa naweza kufanya uchunguzi wa dhania?" Akauliza Daktari akiwa anamtazama huyo kijana kwa namna ya kumuona ni msumbufu na mdharau kazi za watu.




"Nataka ufanye uchunguzi au hata kama usipofanya uchunguzi hizo dalili nilizokupa unaweza kunitengenezea ripoti!"




"Kha! Makubwa! Wewe ni mtu wa namna gani? Unajua niko na majukumu mengi na nimeshakwambia sifanyi kazi ya namna hiyo....? Sifanyi mimi." Akasema Dokta Lumoso Papi Mmbai akiitupa mikono yake hewani kwa kukerwa na jambo lile huku akilitundika koti lake la kidaktari kwenye enga ya mule ofisini.




"Dokta?" Akaita Tally kisha akapiga hatua moja kumsogelea akasema.




"....Hakikisha kazi hii niliyokupa inafanyika usiku wa leo nyumbani kwako kwenye maabara ndogo ya pale kwako, iwe ni siri, sitaki mtu yeyote ajue," akaweka koma na kuchomoa bastola kutoka kiunoni. Akaendelea.




"....Kama mtu mwingine akijua basi hakikisha umeandaa mahali mwili wako utazikwa na ujinunulile Suti kwa ajili ya mazishi yako maana nitakuua. Unaweza kumwambia Dokta Omary Maboli Siki kama kumshirikisha kwani hata yeye amepewa onyo kama hili nikupalo wewe. Kama hutafanya mapema, kesho jioni nitakuja nyumbani kwako na ndiyo inaweza kuwa siku yako ya mwisho kuishi ndani ya mji huu wenye safu ya milima ya Uluguru ambayo inatema hewa safi. Kwaheri Dokta." Tally akatoka baada ya kuirudisha bastola yake kiunoni, Dokta Lumoso Papi Mmbai akabaki akiwa kwenye hali mbaya ya kimawazo, alinyong'onyewa na mwilia akajikuta anajiketisha tena kitini pasipo kupenda. Akajiuliza sana kuhusiana na mtu huyo ambaye kuanzia jina lake hadi muonekano wake vilikuwa vigeni maishani mwake. Alikaa kwa muda mrefu sana bila kupata amuzi la kufanya. Njaa ilikimbia maili nyingi sana na kwenda kujificha chini ya mvuko wa nyongo akahisi kichefuchefu hata hivyo hakutapika, tumbo lilikuwa likiunguruma kama radi iungurumavyo. Amejuaje kama anayo maabara nyumbani? Makubwa!




Mh! Ni Rusu huyu wa uchango wa njaa. Akajiwazia baada ya tumbo lake kuendelea kuunguruma.


Akanyanyuka pasipokujua anataka kutoka au anataka kufanya nini hata hivyo alijikuta malngoni akatoka bila kuufunga mlango wa ofisi yake maana hakuona haja ya kufanya hivyo kama hata akifunga bado kuna watu waliweza kuingia na kumuachia vitisho. Wazo la kuwa alitakiwa kwenye maabara kwa ajili ya uchunguzi lilipotea hakujua mwendo aliokuwa akitembea ni wa maulizo kwa wanaomtazama alijiona sawa kimwili na akili vile atembeavyo huku wanaomuona wakiamini kwa asilimia kubwa lipo jambo lenye kutatisha linalomkabili Daktari huyo. Akiwa anatembea taratibu, macho yakiwa mbele kama Roboti, kwa mbali kwenye korido nyingine ya kutokea kwenye wodi ya watoto, alimuona Dokta Omary Maboli Siki akiwa anatembe kwa mwendo wa kinyonga 'nenda au rudi kama hutaki'. Mwendo ule ukamfanya amtazame kwa kitambo kidogo hata hivyo mwenzake naye alimuona namna alivyokuwa akija na kusita akimtazama. Akasimama naye akiwa anamtazama vivo hivyo, wakatazamana mithili ya watu wenye uhasama kila mmoja akiwa na fikira yake yenye ushabaha na mwenzake. Walitazamana kwa muda hadi pale Omary Maboli Siki alipotikisa kichwa kwa masikitiko na kuondoka.




Siku kwao ilikuwa mbaya, hawakuwa na amani hata kazi ilifanyika chini ya kiwango, kila mmoja alikuwa akisononeka na moyo wake. Dokta Omary Siki alikuwa ni kiburi na mtu anayejiamini sana hakuwa mtu wa kuyumbishwa na vitisho hivyo alichokifanya baada ya kupokea vitisho vya kuuawa endapo atakaidi agizo alilopewa, aliondoka nyumbani kwake alipokuwa akiishi maeneo ya Kichangani Mjini Morogoro hadi Chamwino kwa suhuba wake mkubwa aliyekuwa akifahamika kwa jina moja la Mkude. Alipofika alimtaka faragha suhuba wake huyo wa siku nyingi. Akamueleza yaliyojiri kinagaubaga japo alichoeleza yeye hakikuwa wazi kwani hakuwa amewekwa wazi kama Dokta Lumoso Papi Mmbai. Hiki kikabakia kwenye kifua cha Mkude. Mkude akatoa ushauri suala hilo lifikishwe mezani kwa wanausalama kuhusiana na vitisho hivyo. Dokta Omary akasema kuwa hilo si jambo la kufika kwa polisi kwani huwenda wakawa ni vijana wa mtaani wameamua kuleta fujo tu. Aliamini hivyo kwa kuwa yeye hakufuatwa na mtu mweupe.


Hili likapita.

ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog