Search This Blog

Friday 30 December 2022

HEKAHEKA MSITUNI - 5

    


Simulizi : Hekaheka Msituni 


Sehemu Ya Tano (5)


“Sasa tunafanyaje hapa?” Inspekta Tom Green aliuliza.

“Tunahitaji boti” Latoya aliongea.

SASA ENDELEA

“Tutaipata wapi maana muda unazidi kusonga mbele na nina imani wale jamaa kule kambini watakuwa wameligundua hili na watakuwa tayari wameanza kutusaka?” Inspekta Tom Green aliongea akiuliza.

“Ngoja nichunguze mazingira” Latoya aliongea.
Latoya alianza kuzunguzunguka ukingoni mwa mto akitafuta kama anaweza kupata chombo ambacho kingewawezesha kusafari kwa maji.

“Heeeeey!”

Latoya alipiga kelele akimwita Inspekta Tom Green upande ule ambako alikuwako. Inspekta Tom Green alimbeba Martin na kuanza kwenda kule alikokuwa Latoya.

“Tuna mtumbwi hapa. Nadhani utatufaa” Latoya aliongea akimwonyesha Inspekta Tom Green mtumbwi uliokuwa ukingoni mwa mto.

“Safi sana!” Inspekta Tom Green aliongea huku uso wake ukionyesha tabasamu la furaha. Alimpakia Martin Samweli haraka haraka.

Baadaye Latoya naye alipakiwa na kisha mtumbwi ulianza kuongozwa majini. Safari iliendelea kwa muda mrefu huku Inspekta Tom Green na Latoya wakiwa makini kujikinga na hatari yoyote ambayo ingetokea.

“Mwanipeleka wapi? Ninyi ni akina nani?” Martin Samweli aliuliza. Kwa sasa alikuwa amerejewa na fahamu baada ya kuzimia kwa muda mrefu sana.

“Nadhani habari zetu ulikwishazipata tangu hapo awali. Sina haja ya kurudia tena kuongea kitu ambacho nilikwishakiongea!” Latoya aliongea.

Hapo ndipo kumbukumbu za Martin Samweli zilipomrejea. Alikumbuka kila kitu toka alipovamiwa kule kambini na huyu mwanamke.

“Mmejipalia makaa. Hamtafika kokote kabla Kanali Edson hajawanasa” Martin Samweli aliongea.

“Sisi ni watu tusiokamatika. Safari hii huyo kamanda wako ndiye ambaye atakamatwa” Inspekta Tom Green aliongea.

“Unajidanganya. Tena naamini kwa sasa kamanda atakuwa njiani kuja kuwanasa!” Martin aliongea huku akicheka.

“Wewe ndiye ambaye unajidanganya. Sisi tupo katika kazi hii kwa muda mrefu. Kamanda wako hafahamu hata kidogo kama sisi tuko katika misitu hii. Anachokifahamu ni kwamba wewe umetoroka kambini kwa sababu umeasi jeshi na unakwenda kuungana na serikali. Huo ndiyo ujumbe ambao niliuacha pale kambini. Kwa sababu wazifahamu siri nyingi za jeshi hili basi kwa sasa unasakwa kama dhahabu” Inspekta Tom Green aliongea akicheka.

“Shiiiit! Mmeniangamiza ninyi mbwa. Makoko akinikamata atanichinja kabisa!” Martin aliongea akiporomosha machozi.

“Yes, sasa uamuzi ni wako. Kuendelea na safari ili ukatoe msaada kaw mheshimiwa Rais na ufutiwe makosa yako kisha uishi kwa amani kama shujaa wa Taifa au urudi kwa Makoko kukifuata kifo chako cha kikatili. Na kumbuka kwamba Makoko pamoja na BMM yake mwisho wake ni sasa!” Inspekta Tom Green aliongea.

Martin Samweli hakujibu lolote zaidi ya kubaki akiporomosha machozi. Wababe hawa walikuwa wamemuweza hasa. Alikuwa amebaki njia panda.

Safari ilikuwa ikiendelea katika mto ule. Mtumbwi ulikuwa ukiteleza juu ya maji mithili ya nyoka juu ya majani. Inspekta Tom Green alikuwa akipiga makasia kuuongezea kasi mtumbwi ule. Latoya na Martin Samweli walikuwa wamekaa juu ya mtumbwi ule huku Martin Samweli akiwa bado amefungwa mikono yake kwa nyuma.

Ni wakati huohuo ndipo sauti ya chopa ilianza kusikika ikija upande wao kuufuata mto. Jeshi la Kanali Edson Makoko lilikuwa limeshawakaribia.

“Yes, mambo ni moto sasa. Muda wa kuucheza muziki wetu umekwishakaribia!” Inspekta Tom Green aliongea huku akiiseti vema bunduki yake aina ya AK 47.

“Yes, ngoja tuwaonyeshe namna wababe vile tunafanya!” Latoya alijibu naye akiiseti bunduki yake aina ya AK 47.

“Jamani mnifungue mikono. Nitauawa mimi!” Martin alilalamika akiomba kufunguliwa mikono yake.

“Bado hatujakuamini. Unaweza ukatugeuka. Waonesha una kichwa kigumu cha kuelewa mambo na kuchukua maamuzi sahihi. Hii ndiyo njia salama kwako!” Inspekta Tom Green aliongea.

“We mbwa wewe! Nasema nifun ……..!” Martin Samweli hakuweza kuimalizia kauli yake.

Chopa ya wale waasi ilikuwa imekwishawakaribia. Kombora lilikuwa limeachiwa na lilitua pembeni yao na kufumuka.

“Diiiiiiive!” Inspekta Tom Green alipiga kelele.
Wote walijirusha ndani ya maji pindi kombora jingine lilipotua juu ya ule mtumbwi na kuusambaratisha.

“Ha ha ha haaaaaa! Kwisha habari yao. Halafu kumbe yuko na wengine?” askari mmoja kwenye chopa aliongea.

“Basi leo wameingia choo cha kike!” askari mwingine naye aliongea.

Inspekta Tom Green aliogolea chini kwa chini ndani ya maji huku akiwa amemshika mkono bwana Martin Samweli. Baadaye wote waliibukia ng’ambo yam to mahali ambapo palikuwa na kichaka.

“Yaani wewe kenge ni mnyama kabisa. Utaniua wewe!” Martin alilalamika. Inspekta Tom Green hakujibu chochote.

“Nifungue tafadhali, nitashindwa kujitetea na hawa jamaa wataniua!” Martin aliongea huku sasa machozi yakimtoka.

“Hii ni nafasi yako ya mwisho ya kujisafisha. Ukifanya ujinga tu, basi kumbuka sisi ni zaidi ya shetani!” Inspekta Tom Green aliongea huku akizikata kamba za mikono zilizomfunga Samweli.

Wakati huo huo Latoya alimrushia Martin bunduki aina ya AK 47.

“Ahsante sana. Sasa tuingie uwanjani. Mimi naufahamu vema msitu huu. Nitawaongoza!” Martin Samweli aliongea akiikoki bunduki yake.

Inspekta Tom Green na wenzake walianza kuchanja mbuga ndani yam situ ule. Walikuwa wakikimbia huku wakiongozwa na Martin. Msitu ule kwa sasa ulikuwa umetapaa wanajeshi kila mahali.
*******


Inspekta Tom Green na wenzake walianza kuchanja mbuga ndani yam situ ule. Walikuwa wakikimbia huku wakiongozwa na Martin. Msitu ule kwa sasa ulikuwa umetapaa wanajeshi kila mahali.

SASA ENDELEA

Baada ya mwendo kidogo kuna kikundi cha askari kama saba wa jeshi la BMM kiliwaona akina Inspekta Tom Green. Hapo ndipo mapambano ya risasi yalipoanza. Ilikuwa ni hatari kubwa sana kwani eneo lile la msitu lilipambwa kwa mivumo ya risasi ambazo zilikuwa zikikohoa kutoka katika bunduki za kila upande. Ndani ya dakika kumi mahaini wale walikuwa wamekwishakandamizwa na kupoteza uhai wao. Akina Inspekta Tom Green waliendelea kusonga mbele.

Dakika kumi mbele walikutana na muziki wa kundi la wanajeshi kama kumi na mbili ambao walikuwa na silaha nzito. Inspekta Tom Green na wenzake ndiyo walikuwa wa kwanza kuwaona wanajeshi wale.

“Sasa hapa tunapaswa tutumie akili!” Inspekta Tom Green aliongea.

“Yap!” Martin Samweli alijibu.

“Tunatakiwa tutawanyike. Latoya utajipeleka na kujikamatisha kwa wanajeshi wale. Mimi nitashambulia kutoka kushoto na wewe Martin utashambulia kutoka kulia. Latoya unajua nini cha kufanya ikitokea hali hiyo!” Inspekta Tom Green aliongea.

“Rodger that boss!” Latoya alijibu.

“Haya tutawanyike!” Inspekta Tom Green aliamuru na wote walitawanyika.

Latoya alijipeleka kwa askari wale na kunyoosha mikono juu ishara ya kusalimu amri. Wanajeshi wale walifurahi sana kwani waliona kama wamekwishapunguza sehemu ya kazi yao. Wanajeshi wale walimsogelea Latoya huku bunduki zao zikiwa tayari mikononi.

“Wenzako wako wapi?” mwanajeshi mmoja aliuliza huku akimpiga Latoya ngumi moja ya tumbo.

“Wameuawa!” Latoya alijibu huku akiigiza huzuni.

“Ha ha ha haaaaa! Pumbvu sana. Kazi kwisha!” mwanajeshi mmoja aliongea.

Ghafla mashambulizi ya risasi yalianza kutokea kila upande wa wanajeshi wale. Hapo ndipo Latoya naye alipowaonyesha uwezo wake. Mithili ya umeme alimfuata mwanajeshi mmoja na kumkandika ngumi ya uso na kisha alichomoa bastola iliyokuwa imewekwa katika mfuko wake kiunoni. Alianza kuwacharaza risasi wanajeshi wale huku akijiviringisha huku na huko kuepa risasi za maadui.

Baadaye maadui wote walikuwa chini wakiwa wameuawa. Wazee wale wa kazi walikutana tena na kupena mikono ya pongezi.

“Safi sana Martin!” Inspekta Tom Green alimpongeza Martin.

“Ahsante sana. Sasa tunakikaribia kijiji. Pale kuna bwana mmoja ambaye ana chopa. Tunapaswa kwenda kuiiba chopa ile ili itutoe kutoka hapa msituni maana safari ni ndefu sana kutoka hapa na hakuna namna yoyote ya usafiri tunayoweza kuipata!” Martin alijibu.

“Sawa. Tufanye hivyo pasi kupoteza muda!” Inspekta Tom Green aliongea.

Wote walianza kukimbia kutoka eneo lile walilokuwepo kuelekea kijijini huku wakichukua tahadhari kubwa sana.
******
Kijiji kilikuwa hakina wanajeshi kabisa. Wanajeshi wote walikuwa wameelekea ndani yam situ kwenye uwanja wa vita. Wananchi wote waliambiwa wajifungie ndani kwani kulikuwa na mapigano ambayo yalikuwa yakiendelea. Hali hii ilifanya kijiji kiwe kitulivu kabisa.

Kwa upande wao akina Inspekta Tom Green ilikuwa ni safi kabisa kwani iliwawezesha kufika katika nyumba ya mwanajeshi yule ambaye alikuwa akimiliki helkopta bila ya tatizo.

Kwa bahati nzuri mwanajeshi yule naye alikuwa amekwenda kwenye uwanja wa vita kwa kutumia gari. Akina Inspekta Tom Green hawakupenda kuipoteza fursa ile. Waliifungua milango ya chopa.

Kwa kutumia utundu mkubwa Inspekta Tom Green aliweza kuiwasha chopa ile. Chopa iliposhika moto, Inspekta Tom Green aliipaisha na kuanza safari ya kuuacha msitu ule. Huku msituni wanajeshi waliendelea kuwasaka akina Inspekta Tom Green wakiamini kwamba walikuwa bado wamenasa mle msituni.
*******
Saa nne za usiku Inspekta Tom Green, Latoya pamoja na Martin Samweli waliingia jijini Kano. Moja kwa moja chopa ile ilielekezwa mpaka katika hospitali ya rufaa ya Taifa ya Kano. Maafisa wote wa usalama hawakuamini kile ambacho walikuwa wakikiona. Chopa ilipotua, Inspekta Tom Green, Latoya pamoja na Martin Samweli walishuka. Inspekta Tom Green alianza kumwongoza Martin kuingia hospitali.

“Dokta Morgan, huyu hapa ni Martin Samweli. Naomba kazi ya kuokoa maisha ya Rais iendelee!” Inspekta Tom Green aliongea.

“Ahsante sana Tom. You guys you are the bests!” dokta Morgan aliongea huku akimpokea Martin Samweli na kumwomba amfuate ndani ya hospitali.

Maafisa wote walipiga makofi na kushangilia. Hawakuamini kama Inspekta Tom Green na Latoya walikuwa wameweza kuifanikisha kazi ile.

“Chifu naomba uongee na waziri wa ulinzi na mkuu wa majeshi waweze kutuma jeshi kule Masolo. Wale jamaa wametawanyika ovyo kutokana na moto tuliowawashia. Mpaka sasa wanahaha kutusaka. Huu ndio muda muafaka wa kuwavamia na kuwatawanyisha. Mashambulizi ya anga ndiyo yanafaa zaidi kwa kambi ile!” Inspekta Tom Green aliongea.
“Sawa Tom” Chifu alijibu.

“Na pia wakumbuke kwamba kijiji cha kwanza wanaishi watu wa kawaida. Eneo linalofuata ndiyo kambi yenyewe ya BMM. Watumie ramani hii ambayo itawaongoza vizuri kabisa!” Inspekta Tom Green aliongezea.

“Umesomeka Tom” Chifu aliongea huku wakati huo akiwa ameanza kufanya mawasiliano na waziri wa ulinzi pamoja na mkuu wa jeshi.
******
Ghafla hali ya hewa pale hospitalini ilichafuka. Kanali Edson Makoko pamoja na baadhi ya wanajeshi wa jeshi lake walivamia hospitali ile. Kumbe Kanali Edson Makoko alikuja kutambua kwamba Martin Samweli alikuwa ameshirikiana na akina Inspekta Tom Green na walikuwa wametoroka kule msituni.

Na pia alikuja kutambua kwamba misheni ya kumwua Rais ambaye aliitekeleza hapo awali haikuwa na mafanikio. Rais alinusurika lakini alikuwa mahututi hospitalini. Pia alifahamu kwamba Rais alikuwa akihitaji damu na damu ambayo ilikuwa ikimfaa ilikuwa ni ya bwana Martin Samweli ambaye alikuwa ni askari wake. Na hii ndiyo sababu ya akina Inspekta Tom Green kumtorosha bwana Martin kule msituni Masolo.

Sasa Kanali Edson Makoko yeye mwenyewe aliamua kuja jijini Kano na kuendesha operesheni ya kumwua Rais pamoja na yule askari aliyemsaliti.
*******

Sasa Kanali Edson Makoko yeye mwenyewe aliamua kuja jijini Kano na kuendesha operesheni ya kumwua Rais pamoja na yule askari aliyemsaliti.

SASA ENDELEA

“Code 002 …. Code 003 …. Code 004 and Code 005. Are there?” Inspekta Tom Green aliongea kupitia kifaa chake cha mawasiliano.

“Tunakupata poa kabisa toka huku nje. Yaani huku nje hali ni tete kabisa!” Amina alijibu.

“Sasa mimi nitacheza huku ndani na ninyi mtacheza kutoka nje kuja ndani. Hakikisheni hakuna kiumbe chochote chenye asili ya hawa waasi kinachotoka salama hapa!” Inspekta Tom Green aliongea.

“Rodger that boss!” Hashim alijibu.

“Haya wazee, mambo ni moto. Sasa naomba mwende kwenye chumba cha mheshimiwa Rais mkaimarishe ulinzi huku. Mimi nitacheza nao hawa kunguni na nitahakikisha hawafiki huko!” Inspekta Tom Green aliongea.

“Sawa kijana!” Chifu aliongea na kuwaongoza wenzake huku bastola zao zikiwa mikononi.

Inspekta Tom Green aliwaamuru manesi na madaktari kufunga milango ya mawodi na ofisi. Pia aliwaambia wawatulize wagonjwa watulie pindi yeye anapopambana na wale wahaini. Manesi na madaktari walifanya kama vile ambavyo Inspekta Tom Green alikuwa amewaamuru kufanya.

Wakati huohuo Kanali Edson Makoko pamoja na jeshi lake walikuwa wamekwishaanza kuingia ndani ya hospitali. Huko ndani walipokelewa na Inspekta Tom Green wakati nyuma walisindikizwa na maafisa wale wengine wa BSA pamoja na maafisa wengine wa Idara mbalimbali za usalama.

Polisi na Jeshi la wananchi pia walikuwa wamewasili pale hospitali kuwasha moto. Hakika mambo yalikuwa ni bambam. Ulikuwa ni mpambano mzito sana ambapo askari waasi waliuawa sana. Hakuna hata mmoja ambaye aliachwa. Vile ambavyo walitegemea na kuaminishwa na kamanda wao ilikuwa tofauti kabisa.

Naye Inspekta Tom Green upande wa ndani alizidi kuwashusha na kuwaounguza wote ambao walijaribu kuingia ndani ya hospitali. Hakika moto wa Inspekta Tom Green ulikuwa ni balaa. Hata Kanali Edson Makoko mwenyewe ilifika kipindi alishangaa. Hakutaka kuamini kama Inspekta Tom Green alikuwa ni binadamu wa kawaida.

Mtu wa mwisho kusalia katika jeshi la Kanali Edson Makoko alikuwa ni Kanali Edson Makoko mwenyewe. Na sasa alikuwa amekutana ana kwa ana na Inspekta Tom Green. Na kwa bahati nzuri walikutana kila mmoja bunduki yake ikiwa imeisha silaha.

“Umeniharibia sana. Nitahakikisha nakuua kikatili sana!” Kanali Edson Makoko alifoka.

“Hapa umekutana na mwamba. Nadhani ingelikuwa vema kama ungelikuwa unasali kumwomba Mungu msamaha kwa dhambi ambazo umezitenda. Unayekwenda kufa ni wewe!” Inspekta Tom Green aliongea.

“Haya na tuone sasa!” Kanali Edson Makoko aliongea huku akimjia wanguwangu Inspekta Tom Green.

Kanali Edson Makoko aliachia konde zito ambalo Inspekta Tom Green alilipangua kwa mkono wake wa kushoto. Kanali Edson Makoko aliliachia konde jingine ambapo Inspekta Tom Green alibonyea na kuliepa.

Baada ya hapo Inspekta Tom Green alimbandika Kanali Edson Makoko konde moja tu zito kwa mkono wake wa kulia ambapo Kanali Edson Makoko alishindwa kuyahimili maumivu ya konde lile. Alijishika taya lake kwa maumivu huku akipiga kelele.

Inspekta Tom Green hakutaka kumpa nafasi kabisa. Alirusha teke kali ambalo lilimpata Kanali Edson Makoko tumboni. Kanali Makoko alijikunja na kulishika tumbo lake akiugulia maumivu. Ni wakati huo ndipo ambapo Inspekta Tom Green alianza kumpa dozi ya ngumi na mateke ya mfululizo.

Kanali Edson Makoko alilainika na kuwa zaidi ya mlenda. Inspekta Tom Green alihitimisha mchezo kwa kuukamata mkono wa Kanali Edson Makoko na kuuvunja. Kanali Edson Makoko alilia sana kwani maumivu ambayo aliyapata yalikuwa ni makali sana. Wakati huohuo askari walifika na kumtia nguvuni.

“Wekeni ulinzi wa kutosha sana kwani mtu huyu ni hatari sana. Ana mengi sana ya kuijibu serikali” Inspekta Tom Green aliongea.

Kanali Edson Makoko aliondolewa pale na kupelekwa cjhumba cha matibabu huku akiwa chini ya ulinzi mkali sana wa polisi pamoja na wanajeshi. Baadaye hali ilikuwa tulivu kabisa pale hospitali. Mheshimiwa Rais aliendelea kupewa matibabu. Aliongezewa damu mara baada ya kuitoa katika mwili wa Martin Samweli.
******
MSITUNI MASOLO

Katika msitu wa Masolo nako mambo yalikuwa ni moto sana. Wanajeshi wa Jeshi la wananchi waliuvamia msitu na kuanza kupambana na waasi. Waasi wa kikundi cha BMM walishambuliwa vilivyo na kuteketezwa kabisa. Hawakuwa na pa kukimbilia.

Wale waliosalia walikamatwa na kushikiliwa mateka. Kambi yao iliteketezwa na kusambaratishwa kabisa. Hakuna alama yoyote ya BMM ambayo iliachwa. Na huo ulikuwa ndiyo mwisho wa BMM.
******
Kanali Edson Makoko alifikishwa mahakamani na kusomewa mashtaka ya uhaini. Alionekana na makosa na alihukumiwa kifungo cha maisha gerezani pamoja na adhabu kali sana.
Matibabu ya mheshimiwa Rais Ditric Mazimba yalichukua kama miezi miwili ambapo alirejea kuwa ahueni kabisa.
Bwana Martin Samweli alisamehewa makosa yake na kupongezwa kama mzalendo wan chi ya Bantu kwa kukubali kuokoa maisha ya Rais wake.

Pia Inspekta Tom Green pamoja na maafisa wenzake wa BSA walipongezwa kwa namna ya pekee kwa kazi kubwa ambayo waliifanya. Rais aliwapa shukrani za pekee sana.
Chifu naye alipongezwa kwa kuwapika vijana imara kabisa kwa usalama wa Taifa.
**** MWISHO ***

0 comments:

Post a Comment

Blog