Search This Blog

Saturday 24 December 2022

ULIMWENGU MZIMA KIGANJANI MWA CIA - 4

   http://pseudepigraphas.blogspot.com/2020/06/ulimwengu-mzima-kiganjani-mwa-cia.html

Simulizi :  Ulimwengu Mzima Kiganjani Mwa CIA

Sehemu Ya Nne (4)



Katika Ofisi za CIA kitingoji cha Langley jijini Virginia kuna ukuta wa majina ya Maafisa wa CIA waliotunikiwa tuzo za heshima kutoka na utumishi wao uliotukuka ( Distinguished Intelligance Cross na Intelligence Star), Majina ya maafisa wengi kwenye ukuta huo ni ya wale waliotumikia kitengo cha SAD ndani ya CIA.


Kwa kuzingatia kwamba makala hii inalenga kuzungumzia uhusika wa CIA katika mapinduzi ya serikali ya Cuba kupitia Uvamizi wa Bay of Pigs, Hivyo basi tuone mifano michache sana ya oparesheni zilizotekelezwa na kitengo hiki cha SAD ndani ya CIA, Nitaeleza kwa ufupi ili tusitoke nje ya lengo kuu (mapinduzi ya Cuba ).


Ni idara hii maalumu ya CIA ambayo ilikabidhiwa raia wanne wa Tibet kutoka kwa kaka mkubwa wa kiongozi wa kiroho wa Tibet Mtukufu Dalai Lama ambapo idara ya SAD iliwapa mafunzo ya kikomando watibeti hao kisha wakawarudisha Tibet kutafuta raia wengine 300 ambao SAD iliwapa mafunzo ya kijeshi kwa siri katika kisiwa cha Saipan na mwezi oktoba SAD ikawaongoza wanajeshi hawa mpaka Tibet kuanzisha vuguvugi la kudai kujitenga na China.


Pia ni kikosi hiki maalumu cha idara ya SAD ambacho kilimtorosha kwa siri mtukufu Dalai Lama kwa kupita katikati ya majeshi ya China yaliyokuwa mpakani na kumpeleka India, Mpaka leo haijulikani ni namna gani waliweza kufanya tukio hili, kwakuwa tukio hili awajaliweka wazi mpaka sasa.


Ni kikosi hiki hiki cha SAD ambacho kiliusika na mauaji ya Che Guevara, hii ni kwa mujibu wa nyaraka za siri za CIA zikizowekwa wazi mwaka 2004, ambazo zinaonesha kuwa Amri ya kumpiga risasi Che Guevara miaka ya 1960 ilitoka kwa makomado wa SAD.


Ilikuwaje....


Ilikuwa hivi, Jeshi la msituni lililojiita Jeshi la Ukombozi la Bolivia (National Liberation Army of Bolivia) lilianzisha vita dhidi ya serikali ya Bolivia ambayo ilikuwa inaungwa mkono na Marekani, Jeshi hili likuwa na vifaa vya kisasa na liliungwa mkono na mwanamapinduzi Che Guevara, katika hatua za mwanzo za mapigano, jeshi hili la waasi lilionekana kushinda dhidi ya majeshi ya serikali, ndipo hapo CIA wakatuma makomando wa kitengo cha SAD ambao walienda kutoa mafunzo kwa majeshi ya Bolivia katika milima ya Camiri, Na baada ya hapo wakawaongoza kupigana na waasi na kufanikiwa kuwashinda, na kisha makomando wa SAD wakawaongoza makomando wa jeshi la Bolivia (Bolivia Special Forces) kumkamata Che Guevara ambapo Mara tu baada ya kukamatwa komando wa SAD aliyeitwa Felix Rodriguez akaamuru auwawe.


Hii ni mifano michache kati ya mifano mingi ambayo CIA kwa kutumia kitengo cha SAD wameendesha opesheni maalumu za kijeshi katika nchi nyingi duniani.


Ingawa Rais wa marekani ndiye anayetoa amri ya kufanyika kwa operesheni hizi za kuvamia kijeshi nchi nyingine au kuongoza mapinduzi ya serikali halali duniani kote lakini analindwa na sheria ya Marekani ambayo inampa Rais uwezo wa kukana uhusika wa Rais wa marekani kutoa amri au kufahamu kinachofanywa na kitengo hiki. (Plausible Deniability).


Sheria hii ilitingwa mwaka 1947 na inajulikana kama National Security Act, Pia Sheria hii ilitiliwa mkazo na tamko la rais namba 12333 (Executive Order 12333) lenye kichwa cha habari National Intelligence Activities.


Ni idara hii ya SAD ndani ya CIA ambayo ilihusika pia kuwapatia mafunzo ya kijeshi raia wa Cuba waliokuwa wanaishi uhamishoni na kuwaongoza katika jaribio la kumpindua Fidel Castro, Mapigano haya yakihistoria yalidumu kwa siku tatu na yanajulikana kwa jina maarufu la 'Bay Of Pigs Invasion'.


Jaribio hili la mapinduzi ndio lililo changia kudorara kwa mahusiano kati ya Marekani na Cuba mpaka leo hii, Lakini kutokana na umahili wa shirika hili na uhodari wao ndio maana maafisa wa CIA walimshaishi rais Kennedy kukubali mpango wa kuwatumia makomando hao kwenye uvamizi huo.


Mpaka hapa naamini sasa umeelewa vyema kuhusu hiki kitengo maalumu cha CIA cha Special Activities Division (SAD) namna kinavyofanya kazi, Sasa turejee kwenye simulizi yetu ya uvamizi wa Bay of Pigs.


Washington DC, tarehe 20, February 1961...


Maafisa CIA walipo mshauri Kennedy kuhusu uvamizi huo walimuomba sana kuidhinisha makomando wa SAD kutumika, hatimae Raisi Kennedy alikubali makomando wa SAD kuongoza wapiganaji wa Brigade 2506, lakini pamoja na hayo yote, Rais Kennedy alisisitiza sana kwamba ili kulinda taswira ya nchi ya Marekani yeye kama Rais hatoruhusu Marekani kufanya mashambulizi ya anga kusaidia katika mapambani hayo ya kumuondoa madarakani Fidel Castro, maafisa hao walikubali agizo hilo la Raisi Kennedy lakini walijua baadae wangemshawishi Raisi ili waweze kushinda vita ile.


Kwani CIA walijua fika kwamba hawawezi kushinda uvamizi huo pasipo mashambulizi ya anga wakakubaliana na sharti la Rais Kennedy kwamba hakutakuwa na mashambulizi ya anga, Walikubali hili huku wakiwa na dhamira iliyojificha kwamba mara tu vita hiyo itakapoanza watamshinikiza Rais Kennedy atoe ruhusa ya kufanyika mashambulizi ya anga, Walikuwa wanaamini kwamba lazima Rais Kennedy atakubaliana na shinikizo lao pindi atakapoonyeshwa umuhimu wa mashambulizi ya anga pindi vita ikiwa inaendelea, na lazima atafanya hivyo ili kuepusha Marekani kuaibika kushindwa vita wanayoiunga mkono ili kulinda heshima yao ya kijeshi ambayo ilikuwa inahitajika kuliko kitu chochote katika kipindi hiki cha vita baridi.


Rais Kennedy aliidhinisha rasmi uvamizi huu siku ya tarehe 4 April 1961, takribani miezi mitatu tu baada ya kuingia madarakani, Wapiganaji wapatao 1400 wa Brigade 2605 waliogawanywa katika infantry batalioni zipatazo tano na paratrooper battalion moja waliingia katika pwani ya Cuba iitwayo Playa Girón kwa kutumia boti kutokea Guatemala na Nicaragua siku ya tarehe 13 April 1961, Baada ya uvamizi tu kuanza CIA wakaanza kuweka shinikizo kwa rais Kennedy aruhusu japo shambulio moja la anga la ndege za kivita za Marekani kuharibu miundombinu ya viawanja vya ndege za kijeshi vya Cuba, Kennedy alikataa katakata lakini CIA walipozidisha shinikizo na kumpa angalizo kuwa wasipofanya hivyo kuna uwezekano wa wapiganaji hao kushindwa kutekeleza mapinduzi ya kumuondoa Fidel Castro, Kennedy alilazimika na kuruhusu mashambulio ya anga kwa awamu moja pekee.


Hivyo basi tarehe 15 April 1961 ndege za kijeshi zilizo chini ya CIA aina ya B-26, zenye marubani wavamizi walipewa ndege, ndege zile za kivita zilibadilishwa rangi na kufanana sana na zile za Jeshi la Cuba na pia zilipakwa matope ili zikiwa angani zionekane ni chakavu, kisha ziaenda kushambulia kambi ya anga za Cuba na kufanikiwa kuangamiza asilimia 80 ya ndege za Castro, Jeshi la Anga la Castro lilibakiwa na ndege sita tu na marubani saba, ndege hizo zilishambulia viwanja vya ndege za jeshi la Cuba na hatimaye tarehe 16 April wapiganaji wa Brigade 2506 walivamia rasmi Cuba, Mwanzoni mwa uvamizi huu wapiganaji wa Brigade 2506 wakiongozwa na makomando wa SAD katika CIA walionekana kulidhibiti jeshi la Cuba ambapo mwanzoni mwa mapambano haya upande wa Cuba vikosi vya kijeshi vilikuwa vinaongozwa na José Ramón Fernández.


Baada kuonekana kuwa jeshi la Cuba linazidiwa ujanja na wavamizi hawa waliokuja kufanya mapinduzi, Fidel Castro mwenyewe akaingia katika uwanja wa vita na kumuondoa José Fernández kwenye jukumu la kuongoza jeshi kwenye mapambano haya na kujipa yeye binafsi hilo jukimu la kuongoza wanajeshi, Castro alipo ingia front kuongoza mapambano alitumia mbinu ya falsafa ya mapigamo ya José Mart iitwayo "Siri, Vamia, shambulia, gawanya na miliki", mbinu hii ililifanya jeshi la Cuba kuanza kupata mafanikio.


Baada ya Castro kushikilia usukani wa kuongoza mapambano kwa upande wa jeshi la Cuba, wavamizi wa Brigade 2506 wakiongozwa na makomando wa Marekani walizidiwa ujanja na mbinu zote na wakaanza kupigwa kwa aibu kubwa, mpaka kufika tarehe 19 April, ilikuwa dhahiri kwamba ushindi uko upande wa vikosi vya Cuba, kwani walikuwa wanawapiga wavamizi kwa urahisi kana kwamba wanamsukuma mlevi, Ndipo hapa ambapo CIA wakarudi tena kwa rais Kennedy kutaka aidhinishe mashambulizi mengine ya anga, Safari hii Kennedy alikataa katakata, akidai kuwa dunia nzima itaona uvamizi huu imefanywa na Marekani na sio raia wa Cuba wanaoishi uhamishoni.


Kennedy alihofia kuwa kama Marekani itaingilia mapigano hayo kwa kiwango hicho, kulikuwa na uwezekano wa Urusi nayo kuingilia vita hiyo kusaidia upande wa Cuba, kutokana na mvutano mkubwa uliokuwepo baina yao, Kennedy alihofia kuwa ingeweza kuchochea vita nyingine kati ya Marekani na Urusi, vita ambayo ingeigharimu pande zote mbili na Dunia nzima kwa ujumla na pengine hata kusababisha vita kuu ya Tatu ya Dunia, kwa hiyo Kennedy safari hii akakataa katakata kuidhinisha mashambulio ya anga kwa kutumia jeshi la Marekani.


Joint Chiefs Of Staffs wakaja na pendekezo kwamba litengenezwe shambulio la uongo kwenye pwani ya Marekani na kisha kutupa lawama kwa Cuba ili kuhalalisha mashambulizi ya anga nchini Cuba, lakini bado pia Kennedy alishikilia msimamo wake kwamba hawezi kuidhinisha shambulio lolote la anga kufanywa na jeshi la Marekani, Hapa ndipo ambapo CIA iliumbuka, mkakati wao tangu awali ulikuwa ni lazima mashambulizi ya anga yafanyike ili kuweza kushinda mapigano na kuvishinda vikosi vya Castro na kumuondoa Madarakani, Lakini walimficha kitu hiki Rais Kennedy baada ya kumuona kuwa hasingeli idhinisha uvamizi huo kama wangemuweka wazi kuwa hawawezi kushinda pasipo mashambulio ya anga, hivyo kumficha huko na tegemeo lao la kumshawishi tena kwa mara ya pili yafanyike mashambulio ya anga ndio likawa limegonga mwamba.


Cuba ikaibuka mshindi....................


Tarehe 20 April 1961, siku tatu baada ya uvamizi, wapiganaji waliio patiwa mafunzo na kuongozwa na makomando wa Marekani, ambao waliiovamia nchini Cuba ili kumpindua Fidel Castro waliweka silaha chini na kusarenda kwa vikosi vya jeshi la Cuba, Ilikuwa ni aibu kubwa ambayo haijawahi kutokea katika historia ya jeshi la Marekani, Mateka waliokamatwa na vikosi vya Fidel Castro walihojiwa mubashara kwenye televisheni nchini Cuba na kutoa siri zote namna ambavyo Marekani ilihuiska katika uvamizi huo ambapo Marekani walikuwa wanatafuta sehemu ya kuficha nyuso zao kwa aibu, nchini Cuba taifa zima lilikuwa linasheherekea kwa shamra shamra kushangilia ushindi huo mnono, Fidel Castro aligeuka kuwa shujaa mpya wa Taifa na kujipatia heshima kubwa kimataifa kwa kushinda vita dhidi ya jeshi hatari la 'Marekani' hivyo Fidel Castro akapewa cheo cha juu jeshini cha Fidel Marshall kwa kuyashinda majeshi ya Marekani.


Huko Marekani nako...


Bado bundi alikuwa ndio kwanza ametua, Kila upande ulikuwa unamsukumia lawama upande mwingine, CIA walimuona Rais Kennedy kama ndio kisababishi cha wao kushindwa kutekeleza kwa ufanisi uvamizi na hatimaye kufanikisha kumuondoa madarakani Fidel Castro, CIA walijuta Raisi Eisenhower kutokamilisha mpango huo wa uvamizi kabla ya kuondoka ikulu.


Na kwa upande wa Rais Kennedy aliwaona CIA kama wasaliti kwa 'kumdanganya' na kutompa mkakati kamili tangu mwanzoni kwamba wasingelieweza kushinda vita ile pasipo mashambulizi ya anga, CIA wakamuona Rais Kennedy kama kiongozi ambaye si imara na shupavu au jasiri, na kwa muono wao walihisi kuwa hatoshi kuwa Rais wa Marekani.


Kwa upande wake Kennedy aliwaona CIA kama taasisi iliyopewa nguvu kiasi kwamba imelewa madaraka na kujiona wako huu ya kila kitu na kila mtu. Na moyoni mwake aliamini kuwa hilo linatakiwa kubadilika, Ikumbukwe pia kwamba hapa ilikuwa imepita miezi mitatu pekee tangu CIA wamuue Patrice Lumumba siku ya Tarehe 17 January, 1961 jimboni Katanga, Congo-Kinshasa, Kennedy anafahamika kuwa hakupendezwa na hili tukio lakini kwa kuwa lilitokea kabla hajawa Rais (siku tatu kabla) basi alilimezea mate lakini bado alibaki na kinyongo Kwa hiyo kufeli kwa uvamizi wa Bay of Pigs kuliamsha hasira zake zote alizonazo dhidi ya CIA.


Japokuwa katika umma na hata alipoongea na wanahabari Kennedy alikubali kubeba lawama zote kwa kuwa yeye ndiye aliidhinisha uvamizi huo, lakini pembeni akiwa faragha na wakubwa wenzake alikuwa anaotupia lawama kubwa CIA kuwa ndio waliosbabisha aibu kubwa hii iliyoipata Marekani na jeshi lake, Baada ya hapa mwenendo wa Kennedy ukaanza kubadilika mno. Mwanzoni alipoingia madarakani alikuwa ni tegemezi mno kwa kupatiwa muhtasri wa hali ya usalama wa nchi (Daily Presidential Briefing) kutoka kwa vyombo vya Ujasusi hasa CIA, lakini baada ya tukio la kufeli kwa uvamizi wa Cuba hakutaka tena kupatiwa briefing na CIA badala yake briefings zake zote sasa alizipokea kutoka kwa washauri wa usalama wa taifa (National Security Advisors).


Lakini hakuishia hapo tu, Kennedy kuonesha ni namna gani alikasirishwa alienda mbali zaidi kufanya kitendo ambacho kilipingwa na maafisa wengi wa CIA na wanazi wao, Kennedy alimfuta kazi Mkurugenzi Mkuu wa CIA Bw. Allen Dulles, Katika ulimwengu wa Intelijensia unapomuongelea Allen Dulles hamuongelei tu jasusi, bali ni jasusi mkongwe na mzoefu na wa kiwango cha daraja la kwanza kabisa na mwenye heshima iliyotukuka, Allen Dulles ndiye Mkurugenzi wa CIA aliyetumikia kwa kipindi kirefu zaidi katika historia ya Taasisi hiyo mpaka leo hii (tangu 1953 mpaka 1961), Allen Dulles ndiye aliyesimami mapinduzi ya Waziri mkuu wa Iran miaka ya 1940s (Operation Ajax), Allen Dulles ndiye aliyesimamia mapinduzi ya Rais wa Guatemala mika 1950s, Allen Dulles ndiye aliyesimamia program ya ndege za kijeshi ya Lockheed U-2, Pia huyu ndie aliye simama operation Barracuda iliyo ratibu kifo cha Patrice Lumumba wa Kongo DRC.



ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog