Search This Blog

Thursday 29 December 2022

MIKONO YA JASUSI - 1

  Simulizi : Mikono Ya Jasusi 

Sehemu Ya Kwanza (1)

IMEANDIKWA NA : AHMED JIRIWA


********************************************************************************


Simulizi : Mikono Ya Jasusi 


Sehemu Ya Kwanza (1)




MWANZO




SOMALIA.




Walisalia wanajeshi wawili kwenye jengo ambalo lilikuwa likizidi kuteketea kwa moto na bado mashambulizi ya risasi hayakukoma. Wanajeshi hawa hawakukata tamaa ya kurudisha mashambulizi ya akili ya kuhakikisha kila risasi wanayoitupa inafanya kweli kwa maadui zao, wenzao wawili walikuwa tayari wameshahama kutoka ndani ya jengo hilo na kukimbilia kwenye jengo jingine. Ilikuwa ni zamu ya wanajeshi hao kulihama hilo jengo ili kuweza kukaa mbali na kifo ambacho hakika kilikuwa kimewakaribia kwa hatua chache sana. Milio ya risasi ilikuwa ikisikika kwa sauti kubwa mno na ilikuwa ikitokea kila kona ya eneo hilo. Moto ulizidi kuwaka na moshi mzito ukitanda kila mahali kiasi kuwapa shida ya kupumua. Walichoka sana na jasho jingi lilikuwa likiwatiririka huku miili yao ikiwa imetapakaa damu kwa majeraha kadhaa waliyoyapata kutokana na risasi zilizowapunyua na kuwajeruhi. Mabegi waliyoyavaa migongo mwao waliyaona mazito yanayowaelemea. Ilitisha.




"Tunawalinda hakikisheni hampotezi muda tokeni sasa kwenye hilo jengo muwahi tulipo." Sauti ilisikika kwa kila mmoja kutoka kwenye vipokea sauti vyao walivyovivaa masikioni mwao, wakatazamana usoni kisha wakatikisa vichwa kama ishara ya kila mmoja kuelewa kile kilichozungumzwa na kiongozi wao wa misheni ile ya ukombozi ya kijeshi. Mmoja kati ya wawili wale alikuwa amejibana kwenye kona ya ukuta wa kuelekea kwenye chumba kimoja cha jengo lile na mwingine akiwa chini ya ukuta mfupi wa dirisha lililotoka kufumuliwa dakika thelathini nyuma kwa kombora zito. Mvua ya risasi iliyokuwa ikinyesha ndicho kilikuwa kikwazo kikuu kilichowafanya kushindwa kujitoa kwenye maficho waliyopo. Waliweka mabegi yao vizuri kisha wakazikamatia bunduki zao mikononi na kupeana ishara ya kusonga mbele mmoja baada ya mwingine huku wakijaribu kuwekeana ulinzi. Yule aliyejibanza kwenye kona ya ukuta wa kuelekea kwenye chumba kimoja cha mule ndani akawa wa kwanza kutoka akiwa amejikunja kutokea kiunoni na kukimbia kwa kasi kubwa akiifuata korido nyembamba iliyokuwa ikieleke kwenye mlango wa kuelekea nje kisha akajificha kwenye mlango wa chumba cha pembeni kwenye korido ile ndefu. Huyu mwingine naye akatoka kwa kasi ileile akiwa ameinama vilevile akampita yule wa kwanza na kujificha kwenye mlango wa mbele.




"Mnatusikia...mnatusikia!!" Sauti ya kiongozi wa msafara huo ikasikika tena mara baada ya wao kuwa wamepiga hatua fulani ya kuanza kutoka kwenye jengo lile ambalo hakika lilikuwa likienda kuchakalika kwa moto wa mlipuko.




"Tunasikia na tuko mbioni kutoka." Alijibu mmoja kwa sauti yenye ushupavu mwingi japo hali ilikuwa ni ngumu na yenye kukatisha tamaa. Wakatazamana tena kwa muda kisha yule wa kwanza akaanza kutoka pale mafichoni na kutimua mbio. Ilikuwa ni hatari sana na ilihitaji ujasiri mkubwa kama walionao vijana wale wa kijeshi. Risasi kama mia sita sitini na sita zilikosa kumtungua, alijirusha hewani na kujisereresha sakafuni kama nyoka anayeukimbia moto uliotaka kuyaondosha maisha yake akaukumba mlango ambao ulikuwa umeshachoka kwa kuchakazwa kwa risasi. Akatoka nao nje kisha kwa uwezo mkubwa akajigeuza kimgongomgongo na kuelekeza mtutu wa bunduki yake kule alikotokea huku risasi kadhaa zikimtoka. Alikuwa na lengo la kuwachanganya maadui ili mwenzake aweze kutoka kwa usalama. Alipotulia kidogo yule mwingine naye akatoka mbio akiwa ameinama hadi alipofanikiwa kutoka kabisa nje ya lile jengo. Hawakulaza damu walisimama na kuanza kutimua mbio wakipita kwenye maficho ili wasionekane. Mlipuko mkubwa ukasikika nyuma yao baada ya jengo lile kupokea kombora jingine na hiyo ikiwa ni baada ya wao kurudisha mashambulizi pale mvua ya risasi ilipokuwa ikinyesha kuwaelekea wawili wale. Walirushwa hewani kwa nguvu kubwa ya kombora lile na kutupwa chini huku yowe kali la maumivu likimtoka kila mmoja. Wakasimama na kuendelea kutimua mbio. Walikimbia kwa kasi kubwa sana na sehemu waliyokusudia kufika bado hapakuwa karibu. Ilihitaji ujasiri na roho ngumu kuweza kupita kwenye njia ambazo maadui walikuwa wakipiga risasi nyingi kuliko kawaida.




Walibakisha sehemu ndogo kuweza kufika kwenye jengo la mafichoni ili kuwa pamoja na wenzao.




"AAAAAGHRR!!" Sauti kali ya maumivu ilisikika huku kijana mmoja wa kijeshi miongoni mwa wawili wale akipiga mwereka mkali, vumbi Kali likitimka mara baada ya mguu wake mmoja wa kulia kupata dhoruba ya risasi kutoka kwenye bunduki ya adui yenye nguvu. Alikuwa mwenyewe kwa kuwa yule wa kwanza alikuwa tayari ameshaingia kwenye jengo lile la maficho. Wanajeshi wale wazalendo toka kwenye mataifa mawili yaliyoshirikiana kuunda misheni ile ya ukombozi ya kijeshi; Kenya na Tanzania, walitazamana kwa pamoja huku wakikumbwa na ghadhabu kubwa baada ya kumuona mwenzao akiwa chini akiwa ametulia kimya akihema hovyo.




"Mapambano yetu ni hadi tone la pumzi ya mwisho...!" Walisema kauli hiyo kwa pamoja kisha kijana mmoja akaweka bunduki chini na kuchomoa bastola na kuikamata vema mikononi mwake akawatazama wenzake akiomba ulinzi. Ishara za kijeshi zikatumika kijana yule jasiri akajitoa mule ndani na kukimbilia kule ambako mwenzake alishambuliwa kwa risasi ya mguu. Alifanikiwa kufika alipo mwenzake bila kusumbuliwa na maadui akapiga goti chini na kumuuliza mwenzake kama alikuwa salama.




"Yeah, niko salama japo mguu wangu umepata madhara makubwa sana." Alijibu yule kijana jeshi huku akiuma midomo yake kutokana na maumivu yaliyokuwa yakimuandama.




"Tunayo nafasi kubwa ya kuendeleza mapambano na kushinda, simama." Alionge yule mwingine aliyekwenda kutoa msaada. Alimshika vizuri makwapani na kumsaidia kusimama akamkokota huku wakiwa wameinama. Loh!


Haikuwa bahati kwa upande wao kwani mirindimo ya risasi ilirindima upya na kuwaelekea wao. Yule mwokozi wa mwenzake aligeuka na kujaribu bahati yake katika kurudisha mashambulizi sauti za maumivu zilisikika kuonesha kuwa alikuwa akiwaadhibu maadui hata hivyo ilikuwa ni kazi bure maana maadui hawakuwa wachache. Risasi zikawaandama kwa fujo wakajaribu kukimbia.




"Ongezeni kasi maana tunawadondosha maadui kwa risasi zetu lakini ni sawa na kazi bure, wako wengi sana." Sauti ya kingozi ilisikika ikisema huku sauti za milio ya risasi zikihanikiza eneo hilo hata hivyo badala ya jibu kutoka kwa hawa vijana wawili, lilisikika tena yowe la maumivu.




"Merceliiine...!" Aliita kwa sauti kubwa sana yule kijana mwokozi baada ya mwenzake kumzidi uzito na kumuelemea. Risasi ilikuwa imepenya kwenye mbavu zake na kutokea mbele damu zikiruka juu. Merceline alisimama kwa muda pasipo kupiga hatua mbele, kinywa kikiwa wazi jasho lililochanganyikana na damu likiyameza macho ya kijeshi na kumfanya kuwa na sura iliyopoteza matumaini ya ishindi. Alikuwa akihema kwa nguvu sana.




"Tunasonga kamanda?" Aliuliza yule kijana jeshi mwokozi hata hivyo hakupata mrejesho wowote kutoka kwa Merceline. Akajaribu kumkongoja kwa taabu hata hivyo hakukuwa na muitikio wowote. Punde, risasi nyingine ikachana kwenye uti wa mgo wa Merceline. Hapa hali ilikuwa mbaya zaidi. Msukumo ule wa risasi ukawatupa mbele kwa pamoja, damu zilikuwa zikimtoka Merceline kinywani na puani kwa wingi mno.




"Vipi makamanda?" Aliuliza kiongozi wa msafara ule wa kijeshi akiwa ameyatoa macho yake kwa hofu.




"Merceline...Merceline amepoteza nafasi ya kuwepo kwenye hii operesheni." Alijibu yule kijana huku akipambana na maumivu makali sana ya hasira iliyokuwa imempanda kwa kiwango cha kupita mipaka.




"Ni hatari sana hapo ulipo Deus, hima ondoka hapo wanakuja na wako wengi sana hao wajinga tunajaribu kuwashambulia kwa risasi zetu hata hivyo wana roho ngumu sana wanazidi kuja kwa kasi." Aliongea kiongozi wa msafara huo. Meja Deus Macha alivuta nguvu na kumbeba mwanadada shupavu Merceline begani kisha akaanza kusonga naye kwa kasi kubwa. Hakutaka kumuacha pale hadharani ilikuwa ni lazima aondoke naye na wakamuhifadhi mahala ambapo pangekuwa na usalama zaidi. Uwezekano wa kuondoka na mwili wa mwanajeshi mwenzake ulikuwa mgumu sana kwani risasi za maadui bado zilikuwa zikimuandama. Wenzake wawili waliosalia walikuwa wakijitahidi kushambulia kwa nguvu sana ili kuhakikisha Meja Deus anafika salama na mwili wa Merceline pale mafichoni. Mashambulizi kutoka kwa jeshi la kikundi hiki cha kihalifu yalikuwa makubwa sana kiasi kwamba uwili wao usingeweza kufanya chochote kwa vijana hao ambao hawakuogopa kufa na walioongezeka maradufu, pamoja na kupunguzwa hata hivyo idadi yao bado haikupungua kumi na watano. Meja Deus alizidi kukimbia kwa kasi na alibakisha hatua chache kuweza kuingia kwenye eneo la maficho kabla ya kufika walipo wenzake. Risasi moja ikamchapa kwenye bega akapiga kelele za maumivu hata hivyo alikuwa tayari ameshaingia kwenye njia ya maficho lakini huko huko aliko risasi nyingine ikapiga ubavuni akabakia kuachama kinywa akiwa hoi na mwili wa Mwanajeshi mwenzake ukimzidi nguvu akawa anayumba nao huku na huko, mara apige hatua mbele, mara nyuma, mara kushoto, mara kulia na hatima ya yote akashuka nao chini akipiga goti moja huku damu nyingi zikimtoka kwenye majeraha yale mabaya ya risasi. Kelele ile Iliwashtua wale wanajeshi wawili ambao walikuwa mafichoni kiasi kupelekea mmoja kutokea kule aliko na kukimbilia pale ambapo Meja Deus alishambuliwa.




__________




Kikosi hiki cha vijana jeshi wane kiliundwa mahususi baada ya hali ya kuogopesha kuibuka na kuiandama nchi ya Kenya kuanzia mapema mwaka jana. Mwanzo zilipata kuvuma tetesi kuwa ni kikundi cha kigaidi cha Al-shabab ndicho kinachofanya matukio hayo yasiyomithilika. Kikundi hiki inasemekana kuwa ndicho kilichokuwa kikiwateka watalii wa kigeni na kuwafanyanyia mambo yasiyo ya kibidamu ikiwemo kuwaibia mali zao au hata kuwauwa. Jambo hili limekuwa likileta udhoofishaji mkubwa wa kitalii nchini humo na ilipunguza wageni kwa kiasi kikubwa. Licha ya hayo yote yaliyokuwa yakifanywa na kikundi hicho au kikundi hicho hatari kushutumiwa hata hivyo chenyewe hakikuweka bayana kuhusu kuhusika moja kwa moja na shutuma hizo. Hali ya hofu ikazidi kuibuka kama kujitoa muhanga kwa vilipuzi vya kuvaa mwilini kwenye kadamnasi ya watu na kadha wa kadha ikazidi kushamiri huku wakikataa kuhusika na matukio hayo ya kutishia usalama wa raia.








Hakika na hakika ni kwamba kwa matukio hayo yanayoogopesha wananchi kwa nchi kama Kenya wasingekubaliana nayo kabisa hivyo shutuma zote zikahamia kwa serikali ya Kenya kuwa jambo hilo linalohatarisha usalama wa nchi hiyo limekuwa likifumbiwa macho.




Tunajua kuwa Somalia ni taifa ambalo halina serikali inayoeleweka tangu kutoka katika ukoloni na kubakia kama taifa lililogawanywa japo kwa sasa taifa hilo ambalo linajulikana kama Jamhuri ya Shirikisho ya Somalia. Licha ya kuwa limekuwa chini ya makampuni mbalimbali ya mawasiliano hata hivyo machafuko yasiyokwisha yamekuwa ni kama nembo tambulishi ya taifa hilo. Na vita kubwa mara nyingi huibuka baina ya wanajeshi wa jeshi la Somalia na kikundi hicho hatari cha wanamgambo cha Al-Shaabab. Umoja wa nchi za Afrika wa kutetea amani ulioundwa na nchi za Uganda, Kenya, Djibout, Burundi na Ethiopia ujulikanao kama AMISOM. African Union Mission In Somalia. Umekuwa ukitoa msaada mkubwa sana kwa majeshi ya Somalia dhidi ya kikundi hicho cha wanamgambo. Pamoja na umoja huu wa majeshi ya umoja wa Afrika kuingilia kati na kutoa msaada hata hivyo bado kikundi hiki kimeonekana kuwa na ubishi mkubwa na kikizidi kuibua mashambulizi ya risasi na vilipuzi vya mara kwa mara kwenye baadhi ya miji kama Beledweyne katikati ya eneo la Hiiraan, Kiistratajia, Daynunay ambao upo kilomita 20 mashriki mwa mji wa Baidoa, Moqokori uliyoko yapata kilomita 300 kaskazini mwa mji mkuu wa Mogadishu na mji wa bandarini wa Garad hasa katika eneo la Puntland lenye mamlaka ya ndani ya Somalia na miji yote hii ambayo inavamiwa na kutekwa mara kwa mara inashikiliwa na majeshi ya Somalia. Kikundi hiki kimekuwa kikiusisitizia uongozi wa umoja huu kuwa iwatoe wanajeshi wake nchini humo huku ikitoa vitisho vikali ikiwemo kufanya mashambulizi kwenye kambi za jeshi hilo au hata kuwakamata wanajeshi wa umoja huo na kuwachinja kisha kuweka kwenye mitandao ya kijamii tukio hilo mara baada ya kulirekodi. Adha hii ya uvamizi imekuwa ikiliandama zaidi jeshi la Kenya kwa kuvamiwa kambi yao iliyopo kwenye mji wa Kulbiyow hasa mara nyingi wawapo kwenye doria. Hii ilikuwa ikileta picha gani? Kwanini majeshi mengine yasionekane kushambuliwa zaidi kama ambavyo jeshi la Kenya likishambuliwa na kusababisha madhara makubwa kwenye kambi za jeshi hilo, ikiwemo kujeruhiwa kwa wanajeshi wa Kenya au hata kuuawa kabisa. Hili liliwaumiza sana kichwa hata hivyo maafisa wakuu wa jeshi hawakulifumbia macho waliamua kulipeleka suala hili ngazi za juu kabisa zinazohusiana na umoja huu lakini ikaonekana ni vita tu na kauli mbiu ya utetezi wa hoja hii ikiwa ni 'vita haina macho.'




Utafanya nini ikiwa umejibiwa hivyo? Jibu lilikuwa ni kwamba hakuna msaada kwenye hilo. Ikaonekana kuwa hakuna madhara makubwa ambayo yanapelekea jeshi la Kenya kulalamikia jambo hili na ilionekana kama wao wanatengwa na umoja huu kwani madhara makubwa yamekuwa yakitokea zaidi kwenye kambi zao. Viongozi wa umoja huu wakatoa mifano mingi na kusema kuwa ni madhara makubwa yanapatikana kote. Pia yanawakumba wanajeshi wa Djibouti, yanawakumba wanajeshi wa Burundi, yanawakumba wanajeshi wa Uganda na vile vile yanawakumba wanajeshi wa Ethiopia na zote hizo kambi zao zinavamiwa kwa nyakati tofauti. Hilo likabaki kuwa ni jukumu la umoja huo na maamuzi ya pamoja ya kuwa majeshi yao yawe na nguvu moja ya kupambana na maadui ambao wamekuwa wakilinyanyasa jeshi la serikali ya Somalia na kuleta hofu kwa raia hadi shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch kuingilia kati kutokana na manyanyaso na mateso makali yanayokumba wananchi wa Somalia. Halikuwa jambo la kukubaliana nalo tu hivi hivi na hata Kenya ikafikia hatua ya kutokukubaliana na hili japo hawakuwa wawazi. Taifa la Kenya likafikiri kutoa majeshi yake labda kwenye umoja huu ambao wao wenyewe waliamua kuingiza majeshi yao kama kuusaidia umoja huu ambao unatambulika na umoja wa mataifa na umeafikiwa vema. Ijapokuwa huu wa kuingiza majeshi ndani ya umoja huu ulikuwa ni mpango wa muda mrefu na uliohitaji nguvu hadi kufikia mafanikio ya kukitokomeza kikundi hiki cha wanamgambo wa Al shabab. Lakini sasa waliona kama inakuwa kinyume chake na kumbe imeonekana kuwa kwa nchi ya Kenya kuingiza majeshi yake ndani ya Somalia, kikundi hicho hatari cha magaidi hakikupendezwa nacho kabisa hivyo kuamua kuishambulia zaidi Kenya sambamba na kambi zake nchini humo huku wakisisitizwa kutoa majeshi yao nchini humo kama ponya yao. Kutoa majeshi kwa shinikizo ulikuwa ni udhaifu mkubwa ambao ungelionesha jeshi la Kenya kwa wanamgambo hao na ni jambo ambalo sidhani kama wangeweza kuliafiki kirahisi hata kidogo. Hili likawa gumu hakika na hakukuwa na dalili zozote kuwa Kenya iko tayari kutoa majeshi yake nchini humo kwa shinikizo, jeshi la Kenya ndilo ambalo limefanya kuongezeaka kwa idadi kubwa wanajeshi ndani ya kikosi cha kulinda amani Somalia AMISOM chenye zaidi ya wanajeshi elfu 21 hadi kufikia sasa tangu kuanzishwa kwake mwaka 2007 ambao kwa sasa uko chini ya mkuu wa umoja huo Erancisco Madeira.




Hali ilionekana kuwa mbaya sana kwa upande wa Kenya kutokana na vitisho na mashambulio ya mara kwa mara yaliyokuwa yakiibuliwa nao. Ilileta hofu kubwa kwa wanachi wa Kenya dhidi ya kikundi hicho ambacho mashambulizi yake makubwa yaliegemea katika kujitoa zaidi muhanga na kufanya mauaji ya kutisha. Hali hiyo kwa ujumla ilileta hofu hata kwa nchi ya Tanzania ambao ni majirani hasa sehemu za mipakani kwa upande wa Mombasa hasa kwenye vijiji vya jirani ambavyo vimepakana na mji huu wa Mombasa. Kadiri hali hii ilivyokuwa ikiendelea ndivyo kikundi hiki kikizidi kupata nguvu zaidi kwa kupitia kwa baadhi ya viongozi wakubwa wa kidini wa nchi hizi vamiwa kiasi kupata jeuri isiyomithilika na ikasemekana kuwa walifanya yote hayo kwa kupewa mafunzo makali ya kiimani na ya kijeshi kabla ili kuwa ni miongoni mwa washirika wa kikundi hiki hatari Afrika na tamko lao kuu lilikuwa ni kupambana kwa ajili ya Mwezi Mungu.




Ndipo maafisa wakuu kabisa wa jeshi kutoka nchi hizi mbili walipopanga kukutana wakijadili namna ya kuweza kujisaidia wenyewe. Maafisa hawa wakuu katika ngazi ya jeshi walikutania jijini Nairobi na kuweza kukaa kwa pamoja ili kuweza kutafuta utatuzi. Ulikuwa ni mkutano mkubwa kabisa na wa kwanza wa kijeshi baina ya nchi hizo mbili na uliwakutanisha katika namna ya kupendeza kabisa.




"Sina hakika kama jambo hili litakwisha kwa salama kwa upande wetu!" Alionesha wasiwasi wake afisa huyu mkuu kabisa wa jeshi la tanzania Leous Mipango aliye katika vazi la suti kali ya gharama ya rangi nyeusi iliyoonekana kumkaa vizuri kama ilikuwa ni zawadi yake aliyoikuta mara tu alipoingia duniani kwa mara ya kwanza; alipozaliwa. Wasiwasi huu ulikuwa si wa jambo dogo kabisa kwani mkuu huyu alikuwa na hakika kubwa sana kama atakuwa tayari kutekeleza kilichokuwa kikienda kujadiliwa nao ni wazi hali ya kiusalama kwa nchi yake inaweza kuwa mbaya.


"Hata sasa hali ni mbaya kwani kikundi hiki cha wanamgambo kimekuwa kikifanya mashambulizi ya kushtukiza nchini kwako, japo jambo hili limekuwa likizungumziwa kwa siri na kuwahadaa wananchi wasijue kama wako kwenye hatari ya kuyakosa maisha yao hasa wale waishio kwenye miji hiyo inayoshambuliwa mara kwa mara, ila sioni kama ni zuio la moja kwa moja kama tu hatutaamua kuweka mkakati wa kulizuia kabisa kwa kuliangamiza shina la mti wenye tatizo. Lazima tupambane na hiki kikosi kwa nguvu zote." Afisa mkuu wa jeshi upande wa Kenya alizungumza. Mazungumzo hayo yalionekana kuwa mazito sana na yaliyofanyika kwa siri kubwa hata hivyo hayakuweza kufikia muafaka na ndani yake kukaibuka mjadala mzito ambao ulileta mvutano mkubwa. Upande mmoja haukuona haja ya kufanya hivyo kwani uliamini haukuwa na matatizo na magaidi hao hata hivyo upande huu mwingine ulitoa hoja zake za msingi na ushahidi mkubwa ambao upande wa kwanza ulijivika upofu kuona. Malumbano yalimaliza siku nzima kisha kufikia muafaka majira ya jioni japo muafaka huo haukuwa wa moja kwa moja. Afisa wa jeshi la Tanzania alisema kuwa jambo hilo analipeleka kwa wakuu wenzake wakalijadili kwa kina na kulifanyia uchunguzi kisha watatumwa wajumbe baada ya wiki mbili kwisha. Mkutano huu ukawa umefungwa kwa namna hiyo.




Haikujulikana ni nini kiliamuliwa ingawa siku iliyopangwa kukutana tena ikiwa ni kama mkutano wa pili na wa mwisho wa kuunga nguvu na kutengeneza umoja wa siri wa kijeshi na kuunda kikosi kikubwa cha kupambana na magaidi hao kilitumwa. Mambo yalifanyika kwa usiri ule ule, wajumbe hawa kutokea Tanzania waliingia siku mbili kabla ya mkutano na waliingia kwa njia tofauti wakiwa kama wafanya biashara. Kamanda Michael Libulango akiambatana na mjumbe mwenzake kutokea Tanzania walifika jijini hapo kwa usiri mkubwa. Walipata mapokezi ya siri vile vile na kufikishwa kwenye hoteli mbili tofauti kama ambavyo walitoka Tanzania na kupokelewa jijini Nairobi tofauti. Hakuna aliyekuwa akijua namna ambavyo waliingia na hakuna pia aliyekuwa akijua kuwa wajumbe hao walibeba nini vifuani mwao bali siku pekee iliyokuwa ikisubiriwa ni siku ya mkutano wa mwisho ili ijulikane kama watu hao watakuwa wamekubaliana kuunga umoja huo wa siri wa kijeshi. Kwa upande wa Kenya kulikuwa na wajumbe wawili pia na aliyekuwa akiongoza ni Kamanda Joenes Otieno.




_______




Asubuhi hii ilizizima kwa ubaridi wa Nairobi huku wakazi wake wakiwa wanaonekana wako na mishughuliko yao ya kila siku kama ilivyo ada. Siku hii ilionekana kuwa ni ya kawaida sana hasa kwa wenyeji ila kama ungalikuwa ni mgeni kama akina Michael Libulango, hali kama hii ingalikutatiza. Kilichokuwa kikisubiriwa ni wakati ufike ili mazungumzo hayo muhimu yaweze kufanyika kikamilifu. Maandalizi yalikwisha fanyika ya kutosha na hakukuwa na jambo lenye kutia shaka kwenye hilo. Muda kama ulivyo hausimami basi ndivyo ilivyokuwa, masaa yalikatika na muda ukasonga hadi ilipofika saa tisa alasiri. Gari mbili tofatuti za gharama zilitoka kwenye mahoteli tofauti na kufikia kwenye Hoteli Serena jijini hapo. Hoteli yenye hadhi ya nyota tano ambapo ndipo hasa mkutano huo wa makubaliano ya mwisho ama maazimio ulipopangwa kufanyika. Baada ya muda mfupi mara tu baada ya kuingia kwenye ukumbi maalumu wa mikutano ambao uliandaliwa kwa niaba yao na wahudumu wa hoteli hiyo, walikwenda moja kwa moja na kuketi kwenye nafasi zao na kusikiliza kile kilichokuwa kikitaka kuzungumzwa. Hawa maafisa wa jeshi kutokea hapo nchini Kenya walionekana kuwa na vyeo sawa vya Luteni kanali (Colonel Lutenant) lakini hawa wajumbe wawili kutokea Tanzania wakiwa na vyeo tofauti Michael Libulango akiwa na cheo cha meja jenerali na aliyefuatana naye akiwa na cheo cha Luteni kanali. Kimya kikuu kilishika hatamu ndani ya ukumbi huo kwa takribani dakika zipatazo mbili ndipo kukuru kakara ya ufunuzi wa karatasi hii na ile ulipoanza. Baada ya funua funua hiyo kutoka kwa mwekiti wa wajumbe hao ambae ni mwenyeji, alijikoza kupangusa harara kooni kisha akawatazama wenzake waliyokuwa wakimtazama huku wakiwa na shauku ya kuanza kilichowafikisha hapo. Haikuwa kwa muda mrefu tena baada ya hapo.




"Natumai tuko tayari kuweza kufikisha hiki kilichoachwa na wakuu wetu tamati?" Alianza kwa kuuliza Luteni kanali Joenes Otieno akiwa kama mwenyekiti wa mkutano huo. Akawatazama tena kama anachunguza mahali ambapo hapatakuwa sawa. Kimya kifupi akakifukuza tena kwa kusema;




"Kila mmoja wetu hapa anajua pale ambapo tuliishia hivyo hapana shaka kilichotuweka hapa ni kusikia upande wa wenzetu wamekuja na hoja gani ili tufikie muafaka wa hili. Wajumbe kutoka Tanzania natumai mmekuja na ujumbe wenye manufaa kwetu sote hapa." Akahitimisha kisha akasogeza karatasi pembeni na kunyanyua uso wake uliobeba macho makali akiwazunguushia wajumbe wote hasa wale majirani zao. Meja jenerali Michael Libulango akajikohoza kisha akafunua karatasi moja ambayo alikwenda kuitupia macho kabla ya kunyanyua macho yake kutazama aliko mwenyekiti wa mkutano huo.




"Asante...asante kwa kupokea nafasi hii ya kuzungumza hasa juu ya yale ambayo yaliafikiwa na wakuu wetu huko Tanzania. Niseme kwamba...!




HATARI INAANZIA HAPA AMA? UNADHANI NINI KIMEFANYA ASHINDWE KUENDELEA? NINI KITAKUWA KIMETOKEA NA JE, HII NDIYO SABABU YA MISHENI ILE YA KIJESHI AMA?






Wajumbe kutoka Tanzania natumai mmekuja na ujumbe wenye manufaa kwetu sote hapa." Akahitimisha kisha akasogeza karatasi pembeni na kunyanyua uso wake uliobeba macho makali akiwazunguushia wajumbe wote hasa wale majirani zao. Meja jenerali Michael Libulango akajikohoza kisha akafunua karatasi moja ambayo alikwenda kuitupia macho kabla ya kunyanyua macho yake kutazama aliko mwenyekiti wa mkutano huo.




"Asante...asante kwa kupokea nafasi hii ya kuzungumza hasa juu ya yale ambayo yaliafikiwa na wakuu wetu huko Tanzania. Niseme kwamba...!




SONGA NAYO SASA...


" PUUFU...!" Sauti kali na nyepesi ya mlipuko ilisikika na sekunde hizo hizo moshi mwembamba ukamwagika. Pamoja na kwamba watu hawa walikuwa ni makamanda wenye vyeo vikubwa jeshini hata hivyo hawakuweza kuendana na kasi ya shambulio hilo. Mjumbe mmoja kutokea Tanzania na yule wa kenya walitumia mbinu kali za kuziba pua na midomo yao ili kuweza kuhakikisha wanawalinda wengine na kuwatoa hapo ndani ili waweze kutoroka na mpango huo makhususi wenye maana kubwa na siri nzito. Hii ilikuwa ni sawa na bure, risasi zipatazo saba zikamwagwa kuwaendea wawili wale na risasi zisizo na idadi tambulifu zenye kuwa na shabaha kali zikawachapa wakadondoka chini huku vichwani wakiachwa na matundu mabaya na ya kutisha sana ya risasi hizo. Joenes Otieno na Michael Libulango hawa walichelewa kupambana na shambulio hilo hivyo walijikuta wakipoteza uoni imara na kuona ukungu mbele ya macho yao hatimaye kiza mara baada ya kuvuta ule moshi mwembamba wa sumu. Miili yao iliwawia uzito huku vichwa vyao vikiwa vyepesi sana mithili ya karatasi kiasi kushindwa kufikiri sawasawa miguu iliwanyima nguvu na kujikuta kwa awamu tofauti wakidondoka chini kwa kishindo.


Shambulio baya kabisa hili.


Baada ya kama dakika tatu kupita, waliibuka watu watatu walio katika mavazi ya kuficha sura huku wakiwa wamekamata mitutu ya bunduki mikononi mwao. Walisogea taratibu huku wakiwa na mitungi midogo ya gesi safi migongoni mwao ambayo iliwasaidia kuvuta hewa safi kwa lengo la kupambana na moshi ule mwembamba wenye sumu. Kulikuwa hakuna masemezano bali wawili wenye nguvu waliweka silaha zao mabegani kisha kuisogelea ile miili miwili iliyozidiwa na sumu ambayo ililala pasipo ufahamu, wakaititika na kutoka nayo hadi dirishani ambako kulikuwa na kamba tayari kwa kuwatoa humo ndani. Walikamata kamba wote watatu huku yule wa tatu akiwa amebeba nyaraka zote ambazo walikuwa nazo wajumbe hao. Wakapotelea nje kwa kamba kisha kutoweka kabisa eneo hilo huku wakiwa hawajaacha ushahidi wowote eneo hilo. Kwanini shambulio lilifanyika ndani ya jambo lililofanyika kwa usiri mkubwa namna hiyo, kuna nini nyuma ya pazia...? Sijui.




_________




Kitu ambacho maafisa hawa wa ngazi za juu za jeshi hawakukijua, ni siri kuvuja, kwanini imevuja, nani mvujishaji na kwa maslahi yapi? Hapo ndipo palipo na utata tena utata mkubwa.




Wakati tukio hili likitokea kwa utaalamu na kasi ya umeme, kuna watu upande wa pili walikuwa wakipiga kumbo bilauri zao za mvinyo wa ghali kwa vicheko na bashasha za kuzidi. Hili ndilo ambalo wale maafisa wa ngazi za juu kabisa wa jeshi walioanzisha mpango huu hawakujua, hata hawa wane walipotumwa kama wajumbe wawakilishi wa mpango huo kwa lengo la kufikia muafaka waliwakuta watu hawa wakiwa wapo kwenye mpango madhubuti kabisa wa kufanya shambulio la kutisha. Soga zenye matumaini zilikuwa zikipigwa huku taarifa ya ushindi ikiwa ndiyo pekee inayosubiriwa. Ilikuwa yapata majira ya saa kumi na dakika tano tu kwa mujibu wa saa ya mkononi ya bwana mmoja aliyejitundikia suti safi nyeusi na ghali mwilini mwake huku akiwa na miwani ya kusomea machoni mwake. Alikuwa na sura ya duara akiwa na rangi nyeusi ya kiafrika asili, alivutia kumtazama mtu huyu na sura yake yenye ndevu zilizokatwa mtindo wa 'O' zilificha kabisa mabaya aliyojaaliwa nayo. Alikuwa akicheka mara kwa mara mtu huyu kulingana na namna soga zile zilizoundwa na watu watatu zilivyokuwa zikiwalazimisha kucheka. Pamoja na kuwa walijikita katika soga na vicheko hata hivyo huyu bwana mwenye ndevu alizozikata kwa mtindo wa 'O' hakuacha kuzidi kutazama wakati kila muda. Kila alipokuwa akitazama muda hakuacha kuwatazama wenzake hawa wawili kisha kujikita tena kwenye mazungumzo. Hii hali ya kutazama saa na kujikita kwenye mazungumzo haikudumu sana kwani katikati ya mazungumzo yao aliingia mtu mrefu na mwembamba ambaye hakuwa amependa kuonyesha sura yake zaidi mgongo wake tu. Watu hawa wenye kutangaziwa ughali wa maisha yao kwa namna walivyovaa na haiba yao, walisitisha maongezi na kumgeukia huyu njorinjori.




"Mpango umekwisha tumezikagua kontena pamoja na bidhaa zake, zote hazina shaka na bidhaa ziko safi na hivi ziko safarini kupelekwa kituoni kwa ajili ya kupelekwa kwenye ukaguzi zaidi kabla ya kuingizwa sokoni ama kwenye matumizi. Kontena mbili zilibeba sumu hivyo tukaziangamiza mapema kuepusha madhara ya sisi wenyewe sasa ama baadae." Alizungumza njorinjori huyu kwa lugha yenye mafumbo. Wale mabwana wakatazamana kisha wakaangua tena vicheko kabla hawajamgeukia tena huyu njorinjori.




"Vipi kuhusu njia; alama zilizotumika ni za mwindaji kwenye msitu mpya au...!" Aliuliza huyu bwana mwenye mtindo wa 'O' wa ndevu.




"Hakuna alama, msitu uliotumika ni nyumba ya mwindaji hivyo hakukuwa na kuhofia kupotea kama ambavyo hakukuwa na kuhofia kupoteza windo."


"Ajabu...! Ajabu sana, kazi imekuwa nyepesi kuliko matarajio." Alisema kwa kustaajabu mtu mmoja miongoni mwa hawa wawili ukiacha huyu mwenye mtindo wa 'O' wa ndevu.




"Hakuna kinachoharibika kama mnavyojua kuwa kila kitu kimesukwa kwa ufundi mkubwa na mapema mno, pia msisahau kama mpango huu umepitia kwenye mikono ya Jasusi." Alisema kwa kujitapa huyu njorinjori kisha akageuka na kuondoka. Hawa watatu nao hawakuona haja ya kuendelea kuwepo. Kazi yao ilishakwisha na walitakiwa kuondoka si tu hapo bali nchini hapo kabisa. Maficho hayo yalifanyika kwa takribani wiki nne na walikuwa wakiishi kifahari sana ndani ya Hoteli hiyo ya Eka; Eka Hotel Nairobi. Hoteli ya kifahari ya nyota nne iliyokuwa ikipatikana pembezoni mwa barabara ya Mombasa. Mabwana hawa walikula wakitakacho, walikunywa na kuvaa mavazi ya kuwaacha safi kila siku na vyote hivi walivifanya wakiwa kwenye vyumba vyao walivyofikia ni mara chache sana ndiyo walikuwa wakikutana kwa ajili ya kuzungumza na kupanga mipango kama ilivyo hivi. Bwana yule mwenye mtindo wa 'O' wa ndevu, alinyanyuka wa kwanza kisha akaweka koti la suti yake sawa na kutengeneza ki-ua kilichokuwa kikining'inia kwenye mfuko wake wa suti na kupiga hatua kuondoka eneo hilo huku akiwa ni mwingi wa tabasamu. Ilikuwa hivyo pia kwa hawa wengine wawili na kila mmoja alipitia njia yake na kutoka kwa muda wake.


Mpango ulikwisha.




_________




TANGA; TANZANIA.




Mzee mmoja aliyekuwa amejificha ofisini kwake kwenye kambi moja ya jeshi nchi Tanzania alisimama kwa kasi kubwa mara baada ya kusoma ujumbe wa barua pepe ulioletwa na katibu muhtasi wake baada ya kuchapwa. Mzee huyu alikuwa amechafukwa kwa vyeo kwenye gwanda lake la kijeshi na alikuwa na 'X' na nyota tatu sambamba na ngao ikiwa ni cheo cha Luteni Jenerali. Kusimama kule kulimchukua kama dakika moja nzima ndipo alipojitoa mezani na kuizunguka ile ofisi kwa mapana na marefu yake, hatua ya mwisho ilimfikisha dirishani akasimama kwa muda.




Wametekwa...! Akawaza nafsini mwake hata hivyo hakukuwa na wazo jingine lililokuja na jibu kwa haraka kwani mlango wa ile ofisi ulifunguliwa na aliyemletea ujumbe wa teleksi ndiye aliyekuwa akiingia hapo.




"Mkuu kuna simu yako kutoka kwa General (Jenerali)...!" Alisema huyo dada ambaye naye alikuwa kwenye sare za jeshi. Kamanda huyu mtu mzima alimtazama yule msichana kwa tuo hata hivyo hakuwa ameitilia maanani taswira ya binti huyu sawasawa kwani akili yake bado haikuwa kwenye utulivu. Alizivuta hatua hadi kwenye kiti chake akaketi.




"Niunganishe naye...!" Aliagiza na yule dada akatoka. Punde simu ile ikaunganishwa.




"Hallo mkuu...!" Alisema huyu mzee ambaye aliitwa Leous Mipango mara baada ya simu yake ya ofisi kupata uhai.




"Mipango imeharibika kila kitu kiko uchi...uchi wa mnyama Leous, nini...nini kimefanyika?" Iliuliza sauti nzito simuni.


"Kunahitajika mipango ya haraka na majadiliano ya nguvu yenye maamuzi chanya na ya muda mfupi." Alijibu Leous Mipango mzee ambaye hakuwa amepewa cheo hiki bure tu bali alikuwa ni mwepesi mno kufikiri na kutoa majibu yenye tija.




"Masaa mawili mbele kutokea sasa kutakuwa na kikao hicho unachokizungumzia sasa kwenye ofisi kuu hivyo natumai utawahi kabla ya wakati?"


"Nitatumia helkopta mkuu!" Alihitimisha maongezi hayo kisha akaikalisha simu ile kwenye eneo lake kisha akachukua nakala za nyaraka zile zilizokuwa zimekwenda na wajumbe kwenye mazungumzo ya mahitimisho. Ingawa huko aendako zilikuwapo hata hivyo kama mtu pekee ambaye aliteuliwa kwa mara ya kwanza kwenda kwa mazungumzo baada ya wito na maafisa wenzao au majirani zao wa kijeshi nchini Kenya hivyo hakuwa na sababu za kuacha kiungo muhimu kama kile ambacho kilikuwa ni hatari sana kuingia kwenye mikono ya maadui. Alitoka wanguwangu na kuacha maagizo kwa mhandisi wake makhususi ambaye alipiga simu ya haraka kwa rubani atakayehusika kumrusha hadi makao makuu ya jeshi la wananchi la Tanzania huko Dar es salaam.




_________




Haikuchukua masaa mengi nje ya yale yaliyotakiwa kutumika kwa Luteni Jenerali Leous Mipango kufika kwenye ofisi kuu ya makao makuu ya jeshi. Aliingia moja kwa moja kwenye chumba cha mkutano na kuwakuta wajumbe watano wakuu wa jeshi wakiwa wameshatwaa nafasi zao huku nafasi mbili tu za mbele zikiwa zimesalia ambapo moja ikiwa ni ya kwake na nyingine ikiwa ni ya Jenerali. Wajumbe wale pamoja na kuwa walikuwa ni maafisa wenye vyeo vikubwa jeshini hata hivyo hawakumpata Leous Mipango kwa wadhifa wake hivi walinyanyuka kikakamavu na kutoa salamu za kijeshi kwa mzee huyo; akazipokea na kutwaa nafasi. Kimya kilikuwa ni kiungo pekee kilichokuwa kimewafunika maafisa hawa wa jeshi huku kila mmoja kwa namna yake akitafakari ya kwake kichwani. Leous Mipango alikuwa na mjadala mzito sana kichwani mwake ambao ulibeba ghadhabu kali mno, kila akitafakari anaona jinsi mchezo mchafu ulivyoundwa na bilashaka ulikuwa na maslahi mazito ambayo yaliijaza mifuko ya benki ya wachezaji hao.








Leous Mipango alikuwa na mjadala mzito sana kichwani mwake ambao ulibeba ghadhabu kali mno, kila akitafakari anaona jinsi mchezo mchafu ulivyoundwa na bilashaka ulikuwa na maslahi mazito ambayo yaliijaza mifuko ya benki ya wachezaji hao.




Ni akina nani...?


Hilo ndilo hasa lililokuwa likiacha maswali ndani ya mjadala huo mzito. Wakiwa katika kujadili bado, mlango ulifunguliwa na sauti ya kishindo ya buti la kijeshi ikawa inadhihiri maumivu yaipatayo sakafu ya hapo kwa kupokea mwendo wa ukakamavu wa bwana mmoja mrefu mwenye macho makali aliyelificha tabasamu mbali kabisa na sura yake na kuiacha sura ikiwa imesawijika. Aliingia hapo akiwa ni kama mtu mwenye haraka sana. Alivaa gwanda safi za jeshi sambamba na kofia iliyomkaa vema, gwanda yake ilikuwa na 'X' na nyota nne sambamba na ngao, huyu alikuwa na cheo cha Jenerali ikiwa ni cheo kikubwa sana jeshini. Wajumbe wote mule ndani sambamba na Leous Mipango walisimama kutoa heshima naye kwa kujali alizijibu akaketi kwenye nafasi yake. Aliwatazama wajumbe wote kwa nafasi kisha akainama kwenye meza aliyopo akilifungua jalada moja lililopo usawa wa macho yake.




"Nchi imezizima ghafula...! Nchi imezizima ghafula kwa kile kilichokwenda kutokea huko jijini Nairobi. Tumeitana hapa kwa kuwa kila mmoja anajua nini kilichotokea na hatukuitana hapa kupeana habari ya kile kilichotokea." Akajikohoza mara baada ya kuvuta pumzi ndani kwa jozi ya sekunde Jenerali huyo. Akaendelea.




"...Tuliitana hapa mwanzoni kabla hatujamteua Luteni Jenerali Leous Mipango kuelekea huko ikiwa ni kama safari ya wito kutoka kwa maafisa wakuu wa jeshi wa nchi hiyo, tukapanga mipango na aliporudi tukaitana tena hapa tukajadili nini amuzi letu kwa kile alichokuja nacho na tukafikia muafaka mzuri hadi kupelekea kuwatuma wajumbe wetu huko...tumepata pigo; pigo hili linaweza kutugharimu kwa kukaribisha machafuko hapa nyumbani. Tumempoteza Luteni usu Makame Daudi lakini vilevile Meja Jenerali Michael kwa upande wetu na Kanali Joenes Otieno kwa upande wa Kenya wametekwa. Kwenye shambulio wamepoteza maisha wawili na wametekwa wawili na hawajulikani walipo hadi sasa." Akaweka tuo Jenerali kisha akawatazama wajumbe wale kwa muda. Kimya kikachukua nafasi na kila mmoja akibaki akitafakari na nafsi yake hadi pale alipouvunja ule ukimya kwa mara nyingine.




"Kwa taarifa fupi niliyonayo ambayo imetoka kwa wenzetu nchini Kenya ni kwamba ukumbi ule wa Serena Hoteli umewekwa chini ya uangalizi mkali kwa siri kubwa, hautumiki hadi pale utakapofanyiwa upekuzi wa kina, pia wapelelezi wa nchini humo wameanza kufuatilia kujua maafisa wetu wa jeshi wamepelekwa wapi. Haiwezekani watu hawa watende jambo kwenye hoteli kubwa kama ile ya kimataifa halafu tukio lisionekane hata kwenye kamera za usalama wa hotelini hapo. Hakuna kilichoonekana kamera inasemekana zilizima kwa muda mfupi sana na zilipowaka na kuendelea kufanya kazi, tayari tukio lilishafanyika. Mwili wa Luteni usu Makame Daudi uko angani sasa unakuja hapa nchini, utafikishwa moja kwa moja kwenye hospitali ya jeshi Lugalo kwa ajili ya uchunguzi wa kina kisha baada ya hapo taratibu nyingine zitafuata. Naruhusu maswali machache na chochote chenye kufaa kabla hatujahitimisha kwa ajili ya kusubiri majibu kutoka Kenya." Akanyamaza na kutulia akiyazungusha macho yake kushoto na kulia kabla ya kuyatuliza mbele. Luteni Jenerali Leous Mipango akajikohoza mara baada ya kupewa nafasi.




"Kama tujuavyo kuwa mkutano ule wa mwisho ulibeba makubaliano ya muafaka wa kile tulichokuwa tumekwenda kukipanga. Hatukukubali moja kwa moja kuwa tuko tayari kushirikiana nao kupambana na kikundi cha kigaidi cha wanamgambo wa Al shabab hata hivyo tulitoa siku chache za mafikirio ya mwisho kisha tungetuma majibu kwa njia ya barua pepe na namna ya kuingiza majeshi yetu nchini Kenya kwa ajili ya kupambana na kikundi hicho ambacho kimekuwa kikiwasumbua sana majirani zetu lakini pia kwa upande mwingine wakileta vitisho huko jijini Tanga na kusababisha mauaji ya kutisha hasa mauaji yale ya kutisha yaliyotoke kwenye kijiji cha Kibatini kilichopo pembezoni mwa mapango ya Amboni. Ni kama hatukuwa tumelipa uzito hili jambo kwa kuwa tulishalimaliza kwa kukisambaratisha kile kikosi kilichokuwa kikileta hofu huko kwenye mapango ya Amboni mwishoni mwa mwaka juzi. Pamoja na kwamba Jenerali amesema kuwa tusubiri majibu yatakayotolewa na wapelelezi wa kijeshi hata hivyo niseme tu kuwa hii ni hatari kubwa na inayotakiwa kukaliwa macho. Lazima tuhakikishe tunapanga mkakati imara wa kuzuia lakini pia kukiteketeza hiki kikosi cha watekaji mara tu tutakapogundua ni wapi maafisa wetu wa jeshi wamepelekwa. Hili jambo halikufanywa na malaika kuwa kuna maono walifunguliwa na Mungu lah! Kazi hii imefanywa na binadamu wenye utashi wa kibinadamu kama ambavyo binadamu wengine walivyo. Nini maana ya hili nilisemalo...? Maana yangu ni kwamba ndani ya shambulio hili kuna mvujishaji siri na huyu ametokea ndani ya nchi ya Kenya au pengine yawezekana ni hapa kwetu hivyo ni lazima tuwape majukumu haya wataalamu wa upelelezi kwa pande zote kazi ya kumtafuta huyo mvujishaji siri na sheria kali ipitishwe juu yake. Naamini litawezekana kwa kuwa Mbwa aliburuzapo fupa na kutafuta maficho ya kulihifadhi, wa kuyagundua maficho hayo ni Mbwa wenziwe." Akamaliza kuongea mzee huyo kwa ghadhabu kisha akaketi chini. Lilikuwa ni jambo lililomuingia kila mmoja akilini mwake na halikuwa na chembe ya wasiwasi. Jenerali alitazama upande walipo wajumbe ili kuona kama yupo mwingine wa kuweza kuuliza swali ama kuchangia kama sio kukosoa kilichozungumzwa. Alisimama mjumbe mmoja miongoni mwa wale sita akajikohoza na kuuliza.




"Huwenda hii shutuma ikawa kubwa sana kwetu na tunaweza tukajiingiza kwenye mtafaruku mkubwa hata kimataifa ikiwa tu tutaonekana tulikuwa na nia thabiti ya kuingiza majeshi yetu nchini Somalia kinyume na taratibu. Kama tunavyojua kuwa yapo majeshi ya kulinda amani ya AMISOM, Jenerali unadhani kipo cha kujibu chenye kutuweka mbali na shutuma hizi?"


"Kwani yupo asiyejua kuwa kikundi hiki cha kigaidi kimejaribu kuingia nchi mwetu zaidi ya mara moja...? Hili liko wazi, hata kwenye zile nyaraka tumeliweka wazi hilo. Wala lisikuumize kichwa...ndiyo, sioni sababu ya kuwaumizeni kichwa wakati sisi wenyewe ndiyo tulikaa na kupanga namna ambavyo tungeweza kuingiza majeshi yetu nchini Kenya ambayo yangesaidia Operesheni hiyo maalumu ya kuwasambaratisha magaidi hao. Tusubiri majibu ya uchunguzi unaofanywa ambao kwa imani...!" Sauti yake ilikwama njiani mara baada ya kugongwa kwa mlango wa hiki chumba cha mikutano. Mlango ulipofunguliwa akaingia kijana mmoja aliye katika sare za jeshi huku akiwa na nyota moja kwenye gwanda lake ikionesha kuwa alikuwa na cheo cha Luteni Usu. Alipiga saluti kwa wakuu wake wa kazi kisha akajivuta hadi meza kuu na kuinama kidogo karibu na Jenerali. Alitoa taarifa fulani kisha akageuka na kuondoka huku nyuma Jenerali alitoa ishara ya kutoka kwa muda akatoka na kuwaacha maafisa wale wakitazamana kwa awamu kisha kimya kikapita. Baada ya dakika saba ama nane kupita ndipo mlango ulipofunguliwa na afisa huyo wa ngazi ya juu kabisa ya jeshi akaingia akaelekea ilipo nafasi yake akaketi.




"Majibu yamekuja kutoka kwa wenzetu na ni majibu mazuri." Akanyamaza na kuwatazama huku kila mmoja akionekana kuwa na shauku kubwa ya kutaka kujua nini kitakachokuzungumzwa. Akaendelea.




"...wajumbe wetu waliotekwa wamejulikana walipopelekwa na hii ni kazi kubwa na ya haraka sana ambayo vijana watiifu na makini katika upelelezi wameifanya. Imegundulika kwamba wamepelekwa kwenye mji wa Kismayu ikiwa ni pembezoni kidogo mwa mji huo. Ni mazungumzo mafupi tuliyoyafanya hata hivyo yalikuwa na maana kubwa kwa kuwa tumeweza kufikia muafaka kuwa ni lazima kuanzia kesho tuwe tumetuma vijana wetu nchini Kenya na hao wataungana na wenzao kwa ajili ya kuanza kuifanya Opereshesheni ya Tunawataka wajumbe wetu. (T.W.W). Vijana hao watakuwa makini na wenye uwezo wa hali ya juu na watakuwa vijana wawili tu, ndani ya hao vijana wawili tumekubaliana tumuingize na komandoo mmoja...!"


"Jenerali, komandoo tena...?" Mjumbe mmoja alidakia pale alipokomea Jenerali. Jenerali akamtazama kisha akasema;




"Ndiyo, lazima kikosi chetu cha kuifanya hiyo operesheni T.W.W kiwe na makomandoo wawili na wanajeshi wengine wawili wenye uwezo wa kimakabiliano ya kila namna. Kwanini tumeafiki hivi...? Tumeafiki hivi mara baada ya kufanyika upekuzi wa siri na wa nguvu eneo la tukio. Watendi wa tukio la utekaji hawakuwa watu wadogo kimapambano ni watu weledi wenye uwezo mkubwa mno na kuna uwezekano pia wakawa ni makomandoo."


"Nadhani mtakuwa mmeelewa hasa hadi hapo?" Akauliza huku akiwatazama kwa awamu. Wakaafiki wajumbe hao na hakukuwa na kazi nyingine zaidi ya kupendekeza vijana ambao wangehusika kwa ajili ya kwenda kuunda kikosi kazi. Baada ya muda mrefu wa majadiliano ndipo walipatikana vijana hao ambao wangekwenda kuungana na vijana wengine wawili kutokea nchini Kenya. Vijana hao alikuwapo Meja Deus Macha na Komandoo Hamidu Jumbe na kwa upande wa Kenya majina yaliyoteuliwa yalikuwa ni Meja Merceline Ong'ong'o na Komandoo Rhoda. Kikao hicho kikafungwa na viongozi wale wakubwa wakatawanyika huku wakitegemea majibu mazuri ambayo yangemfurahisha hata Amiri jeshi mkuu.




________




Vijana hao wane wa jeshi walishushwa na Helkopta ya kijeshi pembezoni mwa mpaka wa Somalia katikati ya msitu ambako iliwalazimu watumie usafiri wowote wao kama wao waweze kufika mjini kisha kuchukua usafiri ambao ungeweza kuwafikisha mjini Kismayu kisha kuelekea kwenye mji ambako ndiko inakosadikiwa kuwa wajumbe wawili walikopelekwa. Haikuwapa shida sana kupata usafiri wa roli moja la mizigo, waliomba lifti kama wasafiri wengine tu na haikuwa ngumu kwao kwa kuwa hawakuwa wamevaa mavazi ya kijeshi. Waliingia mjini Kismayu ikiwa tayari ni majira ya saa kumi na mbili za jioni. Hapa hawakutaka kupoteza muda kwani ilikuwa ni lazima usiku mkubwa wa siku hiyo uwakute huko. Walitafuta usafiri na wakapata hata hivyo hawakuondoka kama kundi waligawana. Ilipofika saa nne wakawa tayari eneo husika ambako walikubalina kukutania hapo. Mipango ilipangwa muda mfupi sana na wakakubaliana kuwa walikuwa na masaa matatu tu ya kupumzika na baada ya hapo waingie kazini kwa ajili ya kufanya kile kilichokuwa kimewapeleka. Haikujulikana waligundulika kwa namna gani kama wao wamekuwa ni wageni wasioeleweka ndani ya mji huo kwani baada ya muda wa mapumziko waliokuwa wameupanga kwisha, wakajikuta wakishambuliwa wakiwa hata bado hawajatoka ndani ya jengo hilo kubwa walilofikia ambalo halikuwa likikaliwa na watu. Uzuri ni kwamba walishajiandaa kwa ajili ya kazi hivyo shambulio hilo lilipoibuka wakawa tayari kukabiliana na jambo lolote lile. Komandoo Hamidu Jumbe ndiye aliyekuwa kiongozi wa kikosi hicho alichukua ramani ambayo ilikuwa ndiyo yenye kuweza kuwafikisha mahali jengo walilopelekwa wajumbe wale waliotekwa walipofikishwa. Walipangana kikamilifu kabisa kisha kujibu mashambulizi hayo makali. Yalikuwa ni mapambano ya kutisha ambayo yalitikisa eneo hilo kwa muda mwingi. Ilikuwa ni ngumu sana kuweza kuwatoka watu hao ambao walikuwa wamejipanga kuwaangamiza kabisa hata hivyo vijana hao walitumia mbinu zao kali kabisa kuweza kupambana na ghasia hio ambayo ilikwenda kuwapa hofu kuu.




"Upande huu tumefanikiwa kuwapunguza sana hivyo bila kuchelewa ni muhimu kutumia njia hii kutoka humu ndani!" Alisema Hamidu Jumbe mara baada ya kutenda vema upande wake.








Yalikuwa ni mapambano ya kutisha ambayo yalitikisa eneo hilo kwa muda mwingi. Ilikuwa ni ngumu sana kuweza kuwatoka watu hao ambao walikuwa wamejipanga kuwaangamiza kabisa hata hivyo vijana hao walitumia mbinu zao kali kabisa kuweza kupambana na ghasia hio ambayo ilikwenda kuwapa hofu kuu.




"Upande huu tumefanikiwa kuwapunguza sana hivyo bila kuchelewa ni muhimu kutumia njia hii kutoka humu ndani!" Alisema Hamidu Jumbe mara baada ya kutenda vema upande wake.




"Hata huku njia iko safi." Aliongeza Meja Merceline Ong'ong'o.




"Hapana hiyo njia haitakuwa sahihi kwetu kwa kuwa si njia ya mahali tunapotaka kwenda pia ni karibu sana na yalipoanza mashambulizi hivyo maadui wanaweza kuwa karibu zaidi ni lazima tufuate njia aliyosema kamanda Hamidu." Aliongea Komandoo Rhoda akiwa makini zaidi na mashine yake kubwa iliyokuwa ikifanya kazi ya kutema risasi. Ilikuwa ni bunduki yenye uwezo mkubwa na yenye kubeba mkanda mrefu wa ramia aliouzungusha mwilini mwake; 'PKM MACHINE GUN', na kila mmoja alikuwa na ya namna hiyo. Mashambulizi yalionekana kupungua kwa kiasi kikubwa sana hivyo kuwapa imani kuwa kazi waliyoifanya haikuwa ndogo kilichobakia kilikuwa ni kutoka mahali walipo na kuwaacha solemba. Zoezi la kutoka halikuwa gumu mwani njia waliyopita ilikuwa kimya sana na njiani walikutana na miili mingi waliyofanikiwa kuishambulia ikiwa imelala bila uhai. Walifika mbali kidogo na pale walistaajabu jengo walilopo likichanguliwa kwa bomu lililoibua taharuki kubwa sana nyuma yao.




"Mungu wangu...!" Alihamaki Meja Deus Macha.




"Imekuwa ni bahati kwa upande wetu na walipoona wanazidiwa nguvu imewabidi kutumia mabomu ya kurusha kwa mkono sasa kazi ipo na wameshajua wanapambana na watu wa namna gani." Alisema kamanda Rhoda. Iliwabidi kukimbia kwa kasi kubwa na tahadhari ya hali ya juu sana ndani ya kichaka kidogo hadi walipofika kwenye jangwa dogo ndipo wakaanza kutembea. Walitakiwa kulimaliza hilo jangwa ndipo waingie mahali wajumbe hao walipohifadhiwa.




Walifika bila kupata ghasia yoyote ila ugumu ukaibuka tena mahali hapo huku yakiwa yameshaingia mapambazuko. Ni kama walikuwa wakisubiriwa kufika mahala hapo, walipokewa kwa mirindimo ya risasi na maadui zao walionekana wakija kwa kasi wakishuka kutokea kwenye miinuko ya michanga mingi huku wakitimua vumbi.




"Tunagawana wawili wawili...!" Alisema kamanda Hamidu Jumbe hata hivyo walikuwa wameshagawanyishwa na risasi zile zilizokuwa zikiwaandama. Wakajikuta namna hii, komandoo Hamidu akiwa na Komandoo Rhoda huku Meja Merceline Ong'ong'o na Meja Deus Macha wakiwa upande wao. Hili nalo lilikuwa ni shambulio la ghafula japo katika medani za kivita kama hivi huwa ni kawaida kushambuliwa kwa kushtukizwa. Hawa makomandoo wawili kwao ilikuwa ni wepesi zaidi kuweza kupambana na kutafuta njia hadi walipofanikiwa kuwaacha maadui zao mbali kisha kukimbilia ndani ya jengo ambalo lilikuwa mbali na hapo kidogo huku wakishuhudia jinsi wenzao wakiwa wanapambana kwa nguvu kubwa.




"Lazima tukaongeze nguvu kamanda!" Alisema Rhoda akimwambia kamanda Hamidu.




"Walipo wanaweza kufika hapa tulipo, tayari wameshapata upenyo." Alijibu Kamanda Hamidu Jumbe aliwaona wenzake walivyokuwa wakipambana na kukimbia wakiingia kwenye jengo moja la hapo. Mbio walizokuwa wakizikimbia hawa vijana jeshi zilikuwa kali sana na za kupendeza sana kwa namna walivyokuwa wakikimbia kufuata uelekeo wa wenzao huku wakiwa wanashambulia na kuwadondosha maadui zao.




"AAAAHGRR...!" Alipiga yowe kali Meja Deus Macha kisha alipinduliwa chali kisha akatupwa chini na kubingilia kwenye mteremko mdogo wa mchanga. Alitupwa huko na huko akipigishwa sarakasi vumbi kali likiibuka eneo hilo.




"Deuuuss...!" Aliita kwa sauti kali Marceline akiwa amefanikiwa kujibana kwenye kijmchuguu cha mchanga ule wa jangwani huku bunduki yake akiwa ameikita kwenye ule mchanga na kutokea upande wa pili hasa kule yalikokuwa yakitokea mashambulizi. Akachungulia kwa chati na kuona wanamgambo wale wa kigaidi wakitimua vumbi timu timu wakiendelea kuwafuata kwa kasi ya kuogofya! Wakishambulia hovyohovyo. Akaruhusu risasi ziwaendee wale magaidi na kweli alifanikiwa kumkinga Meja Deus Macha ambaye alikuwa akishambuliwa zaidi huko alikoangukia. Aliwapunguza kwa kiasi kikubwa wale wanamgambo wa kigaidi na kuwafanya watawanyike kama kundi la ndege lililorushiwa jiwe. Hii ikawa rahisi kwa Meja Marceline kuchomoka pale na kumfuata Mwenzake.




"Are you ok...?"


"Yes, i'm ok...!" Akajibu huku akisimama.




"Risasi ilipiga kwenye begi mgongoni na bila shaka ilipiga kwenye kasha la kuhifadhia risasi maana niliisikia ikitoa sauti kali sana. Huwenda mpigaji hakuwa mbali sana na alikosa lengo la upigaji." Alieleza Meja Deus Macha huku akijinyanyua na kuanza tena mbio kuipanda miinuko ile. Wakiwa wamefika juu na kutaka kulivuka bonde, walisikia tena risasi na walipogeuka nyuma waliwaona maadui zao wakidondoka chini. Hii ilikuwa ni salama kwao kwani wenzao walikuwa wakijaribu kuwapa msaada ili kuokoka pale.




Ajabu ni kwamba vijana wale wa kundi la wanamgambo wa Al shabaab walizidi kuwa wengi na haikujulikana walikuwa wakiibukia kutokea wapi, mashambulizi yalikuwa ni makubwa sana na yalibadilika mfumo. Silaha za milipuko ndizo zilizokuwa zikitumika zaidi. Walipigwa na bomu moja lililowakosa na kuwarusha mbali na kwa kuwa halikuwapa madhara hawakukaa walipotelea kwenye kichaka kidogo na kuingia kwenye jengo ambalo wenzao walikuwapo hapo. Bahati haikuwa kwao hata kidogo wakati wanaingia tu ndani ya lile jengo, mlipuko mwingine ukasikika na kumega upande mmoja wa lile jengo. Kamanda Rhoda alinyanyua silaha yake na kumlenga yule aliyekamata kombora na kumtupa mbali kisha akatulia na kutazama kwa umakini walipo maadui zao. Akiwa hapo kwa umakini mkubwa aliweza kuona mtu mmoja miongoni mwa wale akiwa ameshika bomu la kutupa kwa mkono. Akampima shabaha na kumlenga akalifumua lile bomu kutoka mikononi mwa yule jamaa na kusababisha mlipuko mkubwa sana kwa kikundi kile.




"Safi sana nadhani tumewapunguza vya kutosha na hatuna muda wa kupoteza tena kuanzia sasa ramani yetu inatuambia kuwa tumebakisha hatua chache hadi kufika kwenye jengo ambalo wajumbe wale walihifadhiwa." Aliongea kamanda Hamidu Jumbe mara baada ya kuwa wamefanikiwa kuwatawanya kwa mara nyingine.




"Lakini hapa si salama kabisa na ni hatari kubwa sisi kuendelea kuwepo, hawa watu ni wabishi na wanaweza kurejea kwa haraka sana...lazima tuhakikishe tunafika upande wa pili wa eneo hili baada ya kuvuka kichaka hicho hapo chini." Alizidi kueleza kamanda Hamidu Jumbe mara baada ya kuwa wote wane pamoja. Walikubaliana hata hivyo haikuwa kwa kuondoka kiennyeji waliondoka kwa mtindo uleule wa kulindana na walikubaliana waondoke kama ilivyo awali walitangulia hawa makomandoo wawili ili kuweza kuweka ulinzi kwa hawa wengene wawili wakiwa kule mara tu watakapo kuvuka. Hatari ilianzia hapa, hapa ndipo hofu na woga wa kuzidi ulipoibuka maana vijana jeshi hao wawili ndipo walipozidiwa nguvu na kushambuliwa vibaya sana kwa risasi zile za maadui.


Na hivyo ndivyo ilivyokuwa.




________




Pamoja na kamanda Rhoda kufika mahali kelele za mwenzao ziliposikika hata hivyo alikuta hali ikiwa mbaya zaidi akatoa ishara na mwenzake akafika eneo hilo la tukio na kutoa msaada. Meja Merceline Ong'ong'o hakuwa hata akitikisika hii ilimaanisha kuwa mwanajeshi huyo wa kike alishapoteza maisha.




"Uko salama kamanda...! Aliuliza Hamidu Jumbe. Jibu halikutoka kwa Deus Macha zaidi ilikuwa ni damu nyingi iliyokuwa ikimtoka kijana huyo maeneo yale mawili yaliyojeruhiwa kwa risasi za maadui na kinywani pia damu ilikuwa ikimtoka. Hamidu alimnyanyua kijana yule na kumsimamisha. Deus Macha alipiga kelele za maumivu kwa kitendo kile.




"Jikaze kamanda tutoke hapa...!" Alimwambia.




"Ni...niacheni...nyinyi nendeni bado...bado mnakazi kubwa sitafika mahali po...popote mimi...!" Alilalama Meja Deus Macha huku akiuma meno yake kwa namna maumivu makali yalivyokuwa yakimtembea mwilini mwake. Wakiwa hapo, walisikia sauti za maadui zao zikiwa karibu zaidi. Hakukuwa na namna zaidi ya kuwabeba wote wawili na kuondoka nao eneo hilo. Walifika mbali zaidi kisha wakawasiliana na kambi yao moja kwa moja iliyoratibu mpango huo. Hali ya meja Deus haikuwa ya kuleta matumaini kwani hadi wanamfikisha mahali walipokusudia kuwafikisha kwa ajili ya maficho yao, tayari alishapoteza fahamu.




"Hana muda mrefu atapoteza maisha." Aliongea Rhoda.




"Wamepambana kufa na kupona, hapa walipofika panatosha sana japo haikuwa lengo. Hatuna budi kuimaliza ngwe hii hadi mafanikio." Alijibu Hamidu.




"Tuondoke hapa tuwapoteze maboya kwani wanaweza kufika hapa halafu tukaharibu kila kitu kwani hawatakiwi kuonekana kabisa hawa, inaweza kuwa hatari kubwa kwetu na kwa mataifa yetu. Lazima waje wachukuliwe wakiwa hawajatambulika." Alionge Rhoda. Wakapangana namna ya kufanya kisha wakaondoka hapo wakiwa wamekubaliana kuwashambulia kimya kimya bila sauti, ilikuwa ni lazima kutumia silaha ambazo hazisababishi sauti. Walifika mahali ambapo walipanga kuwashughulikia kwani hapo palikuwa na muinuko na pande zote walikuwa wakiona. Jinsi walivyokuwa wamejigawa ilikuwa rahisi kuweza kufanya mashambulizi ya nguvu sana. Walisubiri kwa muda mrefu huku kimya kikiwa kikubwa zile sauti za mirindimo ya risasi ikiwa imekoma kabisa. Muda ulikuwa ukiyoyoma kwa kiasi kikubwa na hapo ilikuwa tayari ni saa kumi za jioni mapambano yale yalikuwa ni makubwa na yaliyokula muda mwingi. Hata hivyo pamoja na kuto waona maadui zao, hawakuchoka kuendelea kusubiri huku wakila vyakula vyao wakiwa matumatu kwani njaa ilikuwa ikiwasumbua pia








Muda ulikuwa ukiyoyoma kwa kiasi kikubwa na hapo ilikuwa tayari ni saa kumi za jioni mapambano yale yalikuwa ni makubwa na yaliyokula muda mwingi. Hata hivyo pamoja na kuto waona maadui zao, hawakuchoka kuendelea kusubiri huku wakila vyakula vyao wakiwa matumatu kwani njaa ilikuwa ikiwasumbua pia. Wakiwa hapo katika utulivu, Hamidu Jumbe aliona vivuli vya watu vikiwa vinasogea, akajipindua na kujiweka sawa huju akiikamata vema silaha yake kisha akamtazama kamanda Rhoda aliyoko upande wa pili wa kichuguu cha mcanga akampa ishara wakajiweka sawa kusubiri wajitokeze vizuri. Kikosi kile kidogo hakikuwa na hakika kama watu waliokuwa wakiwashambulia kama wapo hai au walishawaangamiza, kitu kilichowafanya wawe na kutokuamini ni kwamba hadi majira hayo hawakuwa wamefanikiwa kuiona miili ya maadui zao. Wakiwa hapo bila kuelewa kitu, mashambulizi mazito na ya kimya kimya yaliibuka na kujikuta wakihaha hovyo wasijue washambulie wapi na nani wamshambulie. Ilikuwa ni patashika nguo kuchanika hadi wanakuja kujiweka sawa walikuwa wamebakia wawili pekee. Komandoo Hamidu alichukua darubini na kutazama ili kuwaona vizuri. Walikuwa watatu na mmoja walishamjeruhi kwenye mkono hata hivyo alimuona mmoja akitoa radio ya mawasiliano kwa lengo la kuwasiliana na wenzake. Lilikuwa kosa kubwa sana kwani mwanadada mwenye shabaha kali alikuwa amemuona na moja kwa moja aliichangua ile radio na kumchana vibaya sana mkono uliokuwa umekamata ile radio. Kabla hajajificha kwenye kichuguu, risasi nyingine ikamtupa mbali huku ikiacha alama mbaya sana ya tundu kwenye paji lake la uso. Mmoja alipotaka kuhama kujaribu kuifuata ile radio ya mawasiliano. Komandoo Hamidu aliona hii ikawa halali yake. Risasi ya shingo ikammaliza kabisa yule adui. Hofu ikaibuka kwa yule mmoja ambaye hakujua afanye nini. Komandoo Rhoda aliweka bunduki yake chini na kuchukua nyingine ndefu akaifunga kiwambo maalumu na kuiweka sawa huku akitumia lenzi yenye nguvu ya bunduki hiyo matata. Aliangalia kwa umakini mkubwa na alipoangalia upande wa mwenzake pia aliona namna alivyokuwa akiwa makini kuhakikisha huyo mmoja hapati nafasi ya kukimbia. Wakiwa hivyo bado, walimuona akitimua mbio huku akionekana kuchanganyikiwa, Komandoo Rhoda akanyoosha mkono kumpa utulivu mwenzake. Akatabasamu huku akikijaza kichwa cha adui yake kwenye shabaha, kabla hata hajatafuta maficho mengine, kichwa chake kilifumuliwa vibaya sana na kutupwa juu na kubingilia kwenye mchanga akiwa hana uhai. Komandoo Hamidu Jumbe alinyanyua dole gumba na kumpa Komandoo Rhoda. Ilikuwa ni kazi nzuri sana yenye mafanikio kwao.




Ilikuwa ni furaha kubwa kuweza kuwafyeka hawa wajinga kwa kiwango kikubwa sana kwa mara ya kwanza watu hawa wawili walikumbatiana kwa furaha kubwa ya ushindi na walikumbatiana kwa muda mrefu. Walipokuja kuachiana walibaki wakitazamana usoni huku matabasamu yakiwa ni sehemu ya pekee ya kuwafariji. Hamidu Jumbe aliweza kuuona urembo halisi wa mwanadada huyo shupavu wa ki-Kenya. Akiwa mrefu mweusi wa asili aliyejaaliwa kifua kipana kilichobeba matiti makubwa kiasi yaliyofichwa kwenye gwanda la kijeshi lililomkaa poa.




"Tumebakiwa na mita mia sita kutokea hapa hadi lilipo jumba la maficho." Alizungumza Kamanda Rhoda akiwa anatazama ramani ndogo ya kijeshi huku akijitahidi kukwepesha macho yake mbele ya macho ya kamanda Hamidu Jumbe aliyeonekana kuvutiwa naye.




"Hakuna usumbufu tutakaoupata kama tutatumia muda huu kuweza kuvamia hapo kwenye maficho walipofichwa wajumbe wetu ila kabla hatujafanya jambo lolote ni vema tukawasiliana na wenzetu wakajisogeza ili baada ya hapo iwe ni kuondoka tu hili eneo."


"Miili ya wenzetu iwe mahala salama kabla hatujavamia." Alichangia kamanda Rhoda. Hilo likawa halina shaka, shaka iliyobakia ni kwamba wanapata wapi mawasiliano na kikosi kilichopo kwa ajili ya msaada wa mwisho wakishamaliza kazi maana kifaa walichokuwa wakikitumia kwa ajili ya mawasiliano kiliharibiwa vibaya pale alipokoswa na risasi ya mgongoni kisha risasi hiyo kupiga begi lake. Mwanzo alidhani ni kibebea risasi kilichovunjwa kama ilivyo kwa Deus macha, kwake haikuwa hivyo bali kifaa cha mawasiliano ndicho kilichokuwa kimeharibiwa.




"Tunafanya nini kamanda masaa yanakimbia sana na hatuna namna ya mawasiliano." Aliuliza kamanda Jumbe huku akiiweka kofia yake nyekundu ya bereti vema kichwani mwake.




"Kupitia ramani, naona mbele kwa umbali wa mita hamsini kuna kibanda cha mawasiliano cha shirika moja la simu la hapa Somalia nadhani tunaweza kulazimisha kutumia hicho kibanda kuweza kuwasiliana na wenzetu." Alijibu Rhoda.




"Kwanini kiwe mafichoni hivi?" Aliuliza Hamidu.




"Siyo mafichoni. Huu ulikuwa ni mji na watu walikuwa wakiishi humu ila kwa sasa unaonekana kuharibiwa sana kwa mashambulio ya mara kwa mara, tujaribu bahati yetu."


"Tufanye hivyo bila kupoteza muda." Alijibu Jumbe. Wakatoka hapo wakiwa wameweka silaha zao begani huku bastola zao wakiwa wamezifutika mahali rahisi ili kuweza kupambana na rabsha zozote kwa wepesi. Safari haikuwa ya kuchosha kwa kuwa ilikuwa ni ya hatua kadhaa hadi kufika mahali palipo na kibanda hicho cha mawasiliano. Walijificha kwanza kutazama usalama wa eneo hilo ili kuona kama kuko salama. Walitulia kwa dakika moja nzima ndipo waliposogea kukikabili kibanda hicho chakaa sana. kilikuwa ni kibanda cha mtandao wa simu wa SOMTEL likiwa ni miongoni mwa mashirika makubwa ya simu inchini Somalia. Hakikuwa na ubora wa aina yoyote na kilionekana kuvurugwa sana huku baadhi ya vifaa vya mawasiliano vikiwa vimeng'olewa. Uwezekano wa kupata mawasiliano ulikuwa mdogo sana na ulikatisha tamaa. Walijaribu kutazama simu hii na ile kuona kama ingeweza kuwasaidi kufanya mawasiliano hata hivyo ilikuwa ni kazi bure. Walikata tamaa.




Wakiwa hapo walisikia michakacho ya kama kiumbe kilichokuwa kikipiga hatua kusogea eneo hilo, wakahamaki na kuanza kuchungulia huku na kule kuona kuwa hicho kilikuwa ni kiumbe cha namna gani. Walijawa na hofu kuu na hawakupenda kukutwa na kiumbe mtu eneo hilo kwani ilikuwa ni hatari kwa usalama wao. Mioyo yao ilipiga kofi na mapigo ya mioyo yao kwenda kasi mara baada ya kumuona mtu mrefu aliyekuwa amevaa mavazi ya kijeshi akisogea eneo hilo. Alivaa mavazi ya jeshi la serikali ya Somalia hiyo ikawapa hofu zaidi kwani kuonekana na watu wa aina hiyo ni mara kumi ukutane na wanajeshi wa kigaidi. Operesheni yao haikutakiwa kuwa wazi hivyo hawakupendezwa kukutana na watu wa namna hiyo kwenye mazingira ya namna hiyo. Walirudi nyuma na kutafuta namna nzuri ya kuweza kujificha. Mwanajeshi yule mrefu na mwembamba aliyekomaa sura ambaye alikuwa akizirusha hatua zake kulikaribia eneo hilo kibabe zaidi, alifika akaingia na kuyazunguusha macho yake mekundu kila mahali akitazama. Utulivu ulikuwa mkubwa sana kiasi kutomtambulisha chochote kilichomo mule ndani ya kile kibanda. Ukimya ule ulimfanya asitambue kama kulishaingia watu mule ndani. Alisogea sehemu ambapo vifaa vya mawasiliano vipo akawa anavigusagusa huku akitafunatafuna tambuu kinywani mwake. Wakati akiwa anaendelea kugusa ni kama kulikuwa na jambo alilihisi mule ndani ikambidi kuwa mtulivu kwa muda akaacha kabisa zoezi alilokuwa akilifanya na kusogea mbele kidogo na eneo alilopo, akatazama kila pande ya kile kibanda mule ndani huku mtutu wake wa bunduki unaotumia risasi za mkanda uliokuwa umejizungusha mabegani, akiukamatia kwa umakini kabisa kishapo akaushusha mtutu ule wa bunduki na kuelekea mahali vilipo vifaa vya mawasiliano. Hakuwa ameona mtu japo hakujipa imani ya moja kwa moja. Aliungaunga nyaya zilizokuwa zimeachiana huku akiwa hayatulizi macho yake hiyo ilikuwa na maana kuwa hakutaka kile alichokuwa akikifanya kionwe na mtu mwingine. Hakujua kama zoezi lile lilikuwa likionwa kwa udadisi mkuwa na makomandoo wawili ambao walikuwa wamejificha eneo lile. Jambo ambalo liliwapa shida vijana wale ni kwamba inakuwaje mwanajeshi kutoka jeshi la serikali awe katika mazingira yale ya hatari namna ile tena yaliyokuwa chini ya wanamgambo wa Al shabab. Lilikuwa ni jambo ambalo kwa wao hawakuwa wakiliafiki na iliwapa mashaka kuwa huwenda magaidi hao walikuwa wakipata msaada kutoka kwa baadhi ya watu ambao ni wanajeshi wa kiserikali kwa kupitia wasaliti wa namna hii. Hawakutaka kumkurupusha ama kulete kelele ya aina yoyote ile zaidi walipaswa kutulia ili kuona kile ambacho alitaka kufanya. Mwanajeshi yule aliendelea na zoezi lake hadi pale alipokamilisha kisha akaonekana kuangalia hapa na pale akawasha swichi moja ya umeme na kubonyeza tarakimu hii na ile pale kwenye kifaa cha mawasiliano kisha akanyanyua kiwambo cha simu kilichochakaa na kukiweka sikioni. Lugha aliyokuwa akiitumia mwanajeshi yule ilikuwa ni kisomali. Lugha hiyo ilimpa shida sana kamanda Jumbe hata hivyo alipomtazama kamanda Rhoda usoni, kuna matumaini aliyaona. Hiyo ilimtanabaishia kuwa huwenda mwenzake alikuwa akielewa maongezi yale.




"Vipi kuna chochote unapata kutoka kwa huyo jamaa?" Aliuliza kamanda Jumbe kwa sauti ya mnong'ono. Hakujibiwa kama alivyoulizwa badala yake alipewa ishara za kijeshi ambazo zilimaanisha kuwa ni lazima wahakikishe wanamuweka chini yao. Baadae kidogo akamueleza kuwa jamaa alikuwa akitoa maelezo mahali kuwa wanajeshi wao wengi wameuawa kisha wakaendelea kutulia hadi mwanajeshi yule alipomaliza maongezi yake. Akazima umeme na kuchomoa nyaya zote alizounga kisha akarudisha kama awali akageuka akiwa na lengo la kutoka nje. Kamanda Jumbe na Kamanda Rhoda walishapanga namna ya kuweza kumdhibiti pasipo kupiga kelele hivyo wakati anatoka. Kamanda Jumbe akarusha kipande kidogo cha chuma juu ya chuma kingine kilichopo kwenye kona karibu kabisa na alipo kama Rhoda. Ile ilikuwa ni mipango ya awali ya kumvuta adui karibu. Mwanajeshi yule makini na asiyependa kugundulika kama alikuwa pale, akageuka kwa haraka kisha akatazama kwa umakini huku mtutu wake wa bunduki ukiwa tayari kufanya shambulizi lolote pale patakapoonekana kitu kisicho cha kawaida. Aliona kipande kidogo cha chuma kikibingilia chini ya sakafu ile chakavu ya eneo lile mara baada ya kupiga kwenye chuma kikubwa. Akatazama juu kuona kama kimeweza kutoka mahali hata hivyo hakuridhishwa na utazamaji ule, akatazama pembeni mwa eneo lile akaona kuna pembe mahali ilikuwa imefunikwa kwa maboksi makubwa. Kama akapatwa na wasiwasi kulikabili eneo lile eidha kwa risasi zake ama asogee karibu akitazame kile kipande cha chuma chakavu. Vyote hivyo vilikuwa vikitazamwa na watu makini na mahodari wa kuweza kusoma mawazo ya adui kwa wepesi mkubwa hivyo kwa kupitia utazamaji ule wakawa wamejiweka tayari kwa makabiliano ya haraka kabla hakujatokea madhara yoyote kwao. Walimuona akipiga hatua kukisogelea kile kipande cha chuma chakavu huku akiwa makini sana. Alipokaribia mahali kile kipande cha chuma kilipoweka makazi, akasimama kwanza kutazama kila mahali huku kwenye kona ilizibwa kwa maboksi akiwa anatazama zaidi ya mara nyingi. Mawazo yake yalikuwa yakikinzana kwa kiasi kubwa na hakujua kama hapo ndipo komandoo wa kike kutokea Kenya alipojificha na alikuwa akisubiriwa yeye afanye kosa la mwaka. Kosa lililokuwa likisubiriwa lifanywe, likafanywa naye. Akainama ili kukiokota kile kipande cha chuma chakavu kwa lengo la kukitathmini. Hili lilikuwa ni kosa la kusimuliwa. Kamanda Rhoda akichomoka kwa kasi ya hatari kama upanga uchomolewavyo na askari wa kisamurai kutoka kwenye ala yake. Alimkumba yule mwanajeshi kwa kumbo kubwa kiasi silaha yake kuvuka begani na kumtoka mkononi kisha akamtandika ngumi kavu iliyotua juu kidogo ya pua ambayo ilimsindikiza chini mara baada ya kujipigiza ukutani. Kabla mwanajeshi yule hajapata nafasi nyingine ya kusimama, akapokea teke moja kali lililompiga kinywani kiasi kutema mate mazito machafu ya damu na mabaki ya tambuu. Hakusubiriwa afanye ujinga mwingine kwani bastola iliyofungwa kiwambo cha kukinga sauti kutoka kwa kamanda Hamidu Jumbe ilikuwa usoni mwake.




"Ni maslahi gani unayoyapata kutoka kwa hawa magaidi mwanajeshi wewe kiasi ukaamua kulisaliti jeshi lako?" Akauliza kamanda Rhoda kwa lugha ya kiingereza ambayo ilikuwa wazi kwa kila mmoja pale. Aliuliza swali hili kutokana na maongezi aliyokuwa akiyasikia yakiongewa na mwanajeshi huyo kwani hayakuwa yakililenga jeshi la upande wa serikali bali jeshi la magaidi. Ni kama yule mwanajeshi wa kisomali alishtuka kwa swali lile. Huwenda kuna baadhi ya maneno kutoka kwenye swali lile aliyakamata.




"Kenya...?" Akauliza yule mwanajeshi wa jeshi la serikali ya Somalia.




NJOO KESHO ASUBUHI.








Aliuliza swali hili kutokana na maongezi aliyokuwa akiyasikia yakiongewa na mwanajeshi huyo kwani hayakuwa yakililenga jeshi la upande wa serikali bali jeshi la magaidi. Ni kama yule mwanajeshi wa kisomali alishtuka kwa swali lile. Huwenda kuna baadhi ya maneno kutoka kwenye swali lile aliyakamata.




"Kenya...?" Akauliza yule mwanajeshi wa jeshi la serikali ya Somalia. Kamanda Rhoda akabadili lugha na kuzungumza naye lugha ya kisomali kwa ufasaha kabisa. Wakionekana kujibizana hadi pale kamanda Rhoda alipomchapa teke jingine la kifua akatulia.




"Lazima atuambie kila kitu na pia aseme kwanini ameamua kuwa msaliti japo najua ni kazi kubwa sana kupata ukweli kutoka kwa watu namna hii. Wanamgambo wa Al shabab au magaidi wowote wanakuwa ni watu wagumu sana kutoa siri zao na hii ni baada ya wao kupitia mazoezi makali ya kuumiza miili yao kiasi kuwapa sugu miili yao ili kukabiliana na kashikashi zozote zile eidha baada ya kutekwa na kuingia mikononi mwa maadui ama vinginevyo...!"


"Huyu atasema tu usitie shaka...ni wapi patafaa kwa ajili ya mahojiano?" Akazungumza kamanda Hamidu Jumbe kisha akauliza.




"Kwa mujibu wa mazungumzo aliyokuwa akiyafanya na magaidi wenzake ni kwamba hapa hakuna mtu yeyote atakayeweza kufika eneo hili kwa muda huu au hata ujao, yeye ndiye pekee anayechukua doria ya eneo hili na alikuwa akiwapa matokeo ya doria yake wenzake kuhusiana na sisi kama tumekwisha kumalizwa ama ni vipi, nadhani nilikueleza...!"


"Alielezaje kuhusu sisi...?" Akadakia kwa kuuliza kamanda Hamidu Jumbe.




"Anajua kuwa tulishambuliwa pia anajua kuwa wawili kati yetu walijeruhiwa ila hana uhakika kama waliuawa hata. Hadi hapo hajajua chochote tena maana wale wampao taarifa ndiwo tuliowaangamiza pale jangwani na hilo ndilo lililomfanya atoe taarifa ya kuwa huwenda wanajeshi wao wote wameuawa."


"Safi, sasa tunataka kujua ulinzi wa maficho yao pia tujue namna ambavyo wamejipanga ili iwe rahisi kwetu kuvamia." Akaeleza kamanda Hamidu. Punde walifanya zoezi kusudiwa walimfunga kamba mikononi na miguuni kisha wakamfunga kwenye nguzo moja ya chuma iliyopo mule kibandani akiwa amekaa. Kwa namna alivyofungwa katu asingeweza kufurukuta. Muda wote mwanajeshi yule alikuwa akitabasamu kama hakuna jambo la hatari ambalo lilikuwa likienda kumtokea muda mfupi mbele. Kamanda Rhoda akaokota tambara gumu na kuukuu akalishika mkononi kisha kuchutama pembeni ya mwanajeshi yule na kumtandika ngumi moja kali chini ya kifua, mwanajeshi yule alipoachama kinywa chake kwa maumivu Rhoda akamlisha lile tambara na kulisokomeza kinywani huku kamanda Hamidu akiwa amesimama mbele yake akiwa amemnyooshea bastola iliyofungwa kiwambo cha kukinga sauti.




"Anza kumuhoji nadhani hii bastola itatosha kumpa maumivu makali ambayo yatapelekea awe mwepesi kujibu maswali utakayomuuliza." Alisema kamanda Hamidu Jumbe. Maswali yakaanza na yalikuwa yakihojiwa kwa lugha ya kisomali ambayo mwanajeshi yule alikuwa akiielewa kwa ufasaha kuliko lugha nyingine yoyote.




"Maficho yenu yako kwa namna gani ulinzi wake na watu wetu mmewaficha vipi?" Alianza kuuliza kwa namna hiyo Rhoda kisha akalitoa lile tambara kinywani mwa yule mwanajeshi.




"Wakenya ni wasumbufu sana kwanini hamuiogopi Somalia na ulinzi wake na mnazidi kuichokonoa pamoja na kutoa onyo kwa tabia yenu ya kujipendekeza kwa kuwasumbua wana taifa lao...?"


"Hatupigani na Somalia na badala yake tunapigana na magaidi wa kisomali, jibu nilichokuuliza tafadhali muda wa hivyo unavyotaka sisi hatuna."


"Unadhani mimi ni gaidi kama unavyonadi hapa...naonekana kama gaidi mimi, mimi ni mwanajeshi mtiifu wa taifa langu...!"


"UUUGHUU...!"Alipiga yowe ambalo halikupata nafasi ya kutoka mbali pia mara baada ya kuzibwa kinywa chake na kile kitambaa ambacho kilipelekea kukohoa sana kutokana na uchafu wa kitambaa kile. Kipigo cha ngumi tatu za mbavu alichopigwa na kamanda Rhoda kilimfanya aheme juujuu kama jibwa koko lililokimbia mbio nyingi za kufukuzwa na jibwa la mtaa wa tatu kutoka alipo.




"Maficho yenu ya siri yako na ulinzi kiasi gani...?" Akauliza akiweka mzaha kando kamanda Rhoda. Yule mwanajeshi akatabasamu kisha kukenua meno kabisa. Meno yaliyokuwa yameshaathiriwa na utafunaji wa miraa kwa kiwango cha kukithiri.




"...mnadhani ni rahisi kuwashinda vijana wanaopigania haki ya taifa lao na imani yao. Ni vigumu sana kuishinda nguvu ya Mungu mmoja na wa haki aliye juu ya mamlaka yote ulimwenguni ambayo amewapa vijana wanaopambania haki...!" Alitamba yule mwanajeshi baada ya kipigo na zoezi la kulishwa na kutemeshwa tambara kuukuu kila wakati ili kuzuia kelele na kupata wasaa wa kufanya naye mahojiano vizuri.




"AAAAUUUGH...! Mpuuzi wewe unaniumiza ujue nitakuua kwa mikono yangu kafiri mkubwa wewe...!" Alilalamika yule mwanajeshi huku akilitazama goti lake moja ambalo lilivunjwa kwa risasi iliyotoka kwa kamanda Hamidu Jumbe.




"Risasi zitauharibu mwili wako wote pasipo kukutoa uhai zaidi ni kwamba utateseka sana. Sema na usijitie kiburi mwanajeshi wewe?" Aliongea kamanda Rhoda.




"Mtakufa nawaambia nyie makafiri, mtakufa na hamtafika popote au...!" Hakumalizia kubwabwaja kile alichokuwa akikibwabwaja mara baada ya risasi nyingine kusogezwa chemba ikimaanisha kuwa akizidi kuropoka itakwenda kumuadhibu.




"Ulinzi ni mkubwa mno...!" Akajibu yule mwanajeshi akiwa anahema juju juu hofu ya kuumizwa mwili wake zaidi ikimuandama. Wakamtazama huku kimya kikishika hatamu. Usoni alijawa na hofu hata hivyo makomandoo wale walipomtazama kwa umakini wa kikachero wakagundua kuwa jibu lake lilikuwa ni la uwongo. Risasi nyingine ikazama kwenye paja lake la mguu uleule uliokwenda kupata madhara muda mfupi nyuma. Kelele za shida kutokana na kulishwa kitambaa kichafu kila apigapo kelele za maumivu hazikufua dafu na badala yake kitambaa kile kichafu kikampelekea atapike hovyo tu. Hakuna aliyekuwa akimhurumia zaidi ni kwamba risasi nyingine ilipandishwa chemba.




"Nimeshajibu sasa...sasa mnataka...mnataka nini...?"


"Jibu lako ni la uwongo, endapo utajibu jibu jingine la uwongo ni lazima goti la mguu uliobakia lichanguliwe kwa risasi kisha paja tena. Ukiwa mkaidi zaidi utatenguliwa bega kwa risasi kisha sehemu ya msuli wa mkono. Unadhani utaishije ukiachwa na majeraha ya namna hiyo?" Akazidi kumpa hofu kamanda Rhoda na sura zao kila alipoziangalia zilionesha wazi kuwa haziko na masikhara ndani yake.




"Ulinzi si mkubwa sana, wapo walinzi wachache ambao wanalinda jengo hilo la mahojiano na mateka hadi amri ya kuwauwa wale watu wenu itakapotolewa. Wako katika mahojiano ya mwisho maana hawataki kusema yale ambayo walitaka kuyaafiki pale kwenye mkutano japo maelezo baadhi yalikuwa kwenye karatasi hata hivyo inaaminika huwenda kukawa na nyaraka zaidi ya zile na viongozi wetu pia wanaamini yapo zaidi ya hayo." Akajibu yule mwanajeshi kisha haraka sana akamtazama yule aliyekamata bastola ambaye hadi hapo alishajua kuwa hajui lugha ambayo anaitumia na yule mwenzake anayemlisha tambara kuukuu ndiye aliyekuwa akimtafasiria. Hofu yake ni kujeruhiwa hata anapozungumza ukweli. Jicho kali lenye ghadhabu kutoka kwa kamanda Hamidu Jumbe likamtazama kiasi kumpelekea ameze funda kubwa la mate ya hofu.




"Nazungumza ukweli, nazungumza...nitazungumza...!" Alilalama yule mwanajeshi.




"Anasema ukweli sasa na anasema kuwa watu wetu wapo hai na wanahojiwa japo hawataki kuwa wawazi juu ya mjadala uliokuwa ukiendelea kule hotelini jijini Nairobi." Alimueleza mwenzake kamanda Rhoda hata hovyo hakuweka wazi kuhusiana na inavyosemekana kuwa kuna nyarana hazikuwa mikononi mwa wale wajumbe kisha akamgeukia yule mwanajeshi na kumuuliza swali ambalo aliamini mwenzake angemuuliza kama asingewahi kumgeukia yule mwanajeshi; mateka wao.




"Wapo katika hali gani...?"


"Hali zao ni mbaya sana kiasi kwamba hata vingozi wasipotoa amri ya kuuawa ni lazima wafe ndani ya siku za usoni." Akajibu kisha kama kawaida akamtazama mwenye bastola.




"Kuna walinzi wangapi kwa ujumla...?" Swali hili kutoka kwa kamanda Rhoda hakuwa amelitegemea hata kidogo na vilevile hakuwa tayari kulijibu. Akabaki ametoa macho kisha akajikurupusha na kutaka kupiga kelele afunguliwe. Alisahau kuwa anafanya kosa. Risasi nyingine ikachangua goti la mguu wa pili na kumfanya alie sana. Alilia mno huku akitoa maneno ya kukatisha tamaa, akisema hawezi kusema tena chochote kwa kuwa hana matumaini ya kutembea hata akiwa hai. Haukuwa uwongo kwani kila swali aliloulizwa hakusumbuka kulijibu na akabaki akiwa amefumba macho yake akimaanisha kuwa hayuko tayari kufanya hivyo. Kamanda Hamidu jumbe alimpiga teke kali la shavu na kuokota kipande kirefu cha nondo nyembamba na kukipenyeza kwenye lile jeraha bichi la risasi. Maumivu makali ukichanganya na kuzuiwa kupiga kelele kulimfanya kwa muda mfupi kunyoosha mkono na kusema yuko tayari kuzungumza. Akaachiwa huru akitweta hovyo huku akiwa katika hali mbaya mno. Mateso yale mafupi yalikuwa mabaya na yenye lengo la kuhakikisha wanapata kitu.




"Wa-Kenya mna roho mbaya sana, Waallah nawaapia kwa jina na Mungu mmoja aliye juu na wa haki, nikipona mtafurahi; nitakufa na Kenya yenu...!" Alilalama yule mwanajeshi msaliti huku akitapika vibaya sana, kamanda Rhoda akatabasamu kifedhuli na kumtazama kwa ghadhabu kali hasa alipowakumbuka wanajeshi wenzake wawili Meja Deus Macha kijana jeshi kutokea Tanzania na Meja Merceline Ong'ong'o kijana jeshi kutokea nchini Kenya waliopoteza maisha kwa risasi zilizosababishwa nao. Akamtazama kamanda Hamidu Jumbe kutoa ishara ya kuruhusu risasi nyingine hata hivyo hakuwahi kuachia risasi kamanda Jumbe.






Alilalama yule mwanajeshi msaliti huku akitapika vibaya sana, kamanda Rhoda akatabasamu kifedhuli na kumtazama kwa ghadhabu kali hasa alipowakumbuka wanajeshi wenzake wawili Meja Deus Macha kijana jeshi kutokea Tanzania na Meja Merceline Ong'ong'o kijana jeshi kutokea nchini Kenya waliopoteza maisha kwa risasi zilizosababishwa nao. Akamtazama kamanda Hamidu Jumbe kutoa ishara ya kuruhusu risasi nyingine hata hivyo hakuwahi kuachia risasi kamanda Jumbe.




SONGA NAYO....




"Jumba la maficho ya siri liko na...liko na walinzi wachache sana, wapo walinzi sita pekee wenye silaha ambao wako nje kukilizunguka jumba hilo kwa upande wa ndani wako walinzi wawili ambao wanalinda mlangoni mwa chumba walichohifadhiwa watu wenu kwa mateso makali sana ya kimahojiano...!" Jibu hili likawafanya makomandoo wale wawili watazamane tena kisha kamanda Rhoda akageuka tena kwa mateka wao bila kumueleza chochote kamanda Hamidu Jumbe.




"Hawa wote wanahusika na ulinzi tu au miongoni mwao wapo wanaohusika kwa mahojiano?" Aliuliza kamanda Rhoda. Yule mwanajeshi akamtazama kamanda Rhoda kwa macho ya kukatisha tamaa kisha akamtazama yule mwenye bastola iliyokosa masikhara, alimtazama kwa wasiwasi mkubwa na chuki dhidi yake. Akameza mate ya hofu tena kisha akajibu huku akipambana na maumivu makali ya majeraha mabaya ya risasi miguuni.




"Kuna watu...kuna watu maalumu ambao wameletwa na viongozi kwa ajili ya kufanya mahojiano na watu hao...!"


"Viongozi hao wanaishi wapi?"


"Hapana, hawa hata mimi mwenyewe sikuwahi kuwaona kabisa na sijui wanaishi mahali gani maana hata majina yao ni siri kubwa."


"Miongoni mwa hao walinzi yupo yeyote anayefahamu?"


"Mkimpata huyo aliyeteuliwa na viongozi au hao walioteuliwa kufanya mahojiano na watu wenu basi ni rahisi kuweza kuwajua hao viongozi hata kwa uchache." Alijibu yule mwanajeshi. Walipomtazama kwa umakini machoni, waliweza kugundua kuwa hakuwa akitania kile alichokuwa akikizungumza. Kamanda Rhoda akasimama kisha akamsogelea mwenzake na kumueleza kila kitu kilichokuwa kikizungumzwa nao. Alipokwisha kumuelewesha akaondoka na kwenda kushughulikia mawasiliano ikiwa ni pamoja na kuunga kila kitu kama alivyokuwa akifanya yule mwanajeshi waliyemteka. Baada ya kila kitu kuwa tayari, kamanda Rhoda alianza kuwatafuta wenzao kwa lengo la kuwaeleza yaliyojiri kisha kuwapa maelekezo ya namna ya kufanya. Hakuacha kuwaeleza hata hatua ambayo walifikia. Alipomaliza aliharibu kabisa yale mawasiliano kwa kusababisha shoti kali ya umeme kisha akamgeukia kamanda Hamidu Jumbe.




"Hawezi kuishi kwa furaha kwa hali hii aliyokuwa nayo!" Aliongea kamanda Hamidu Jumbe huku bastola yake ikitema risasi tatu muhimu. Moja ikiwa imechapa paji la uso la huyo mwanajeshi aliyelisaliti jeshi la serikali ya Somalia na kujiunga na kikundi hicho cha kigaidi cha wanamgambo wa Al shabab baada ya risasi mbili kuzama kifuani mwake. Uhai ukawa mbali naye.




_______




Ulikuwa ni mwendo wa nusu saa kuweza kutoka hapo walipo hadi kufika kwenye maficho ya siri ambayo walihifadhiwa wajumbe maalumu wa majeshi ya nchi hizo mbili. Walikuwa wana kila kitu na uelewa wote wa mahali walipokuwa wakienda hivyo kwao haikuwa ni hali ya kupata wasiwasi kwani waliamini kazi wanayokwenda kuifanya haina uzito wa kutisha kwa kuwa jumba hilo halikuwa kambi ya wanamgambo hao na badala yake yalikuwa ni kama sehemu maalumu ya kuwahifadhia mateka na kufanya nao mahojiano makali. Kasi yao waliyokuwa wakiitumia kwa kukimbia na kutembea kijeshi zaidi, iliwafikisha mapema mno tofauti na walivyotaraji. Walichafuka kwa vumbi baya la jangwani hasa katika kipindi hicho acha upepo mkali. Kismayu ulikuwa ni mji ambao uko pembezoni mwa bahari hata hivyo kulikuwa na baadhi ya miji ndani ya mji huo ilikuwa kame kutokana na mashambulizi ya mara kwa mara hivyo kuyafanya baadhi ya maeneo kuwa katika hali ya u-jangwa. Jengo lilikuwa limejitenga mno na hakukuwa na jengo lolote karibu na lilipo jengo hilo. Uwezekano wa kuingia hapo ulikuwa ni mgumu sana pasipo kuonwa na walinzi waliyopo eneo hilo. Walijificha kwenye muinuko mmoja wa kichanga huku wakitumia darubini kuweza kutazama namna walinzi walivyojipanga.




"Walinzi wako imara sana Rhoda na inavyoonekana wako macho kila sekunde, tutafanya nini sasa?" Aliuliza kamanda Hamidu Jumbe akiwa amekaza macho yake kwenye darubini.




"Subiri kidogo kamanda." Aliongea Rhoda. Macho yake yalikuwa yakiipitia ile ramani ambayo walikuwa nayo muda wote. Kimya cha muda mfupi kilitosha kuweza kuisoma ile ramani ndogo ya kijeshi ambayo ilikuwa maalumu kwa operesheni hiyo na wakati huyo Hamidu Jumbe akiwa ameyasoma mazingira yote ya jumba hilo.




"Hakuna namna nyingine ambayo tunaweza kufanya kamanda, lazima tuizunguuke hii nyuma na tutokee upande wa kaskazini ambako huko hakuna njia kabisa ambayo wanaweza kuitilia shaka. Huku kote ni kugumu na walinzi wako macho."


"Itatuchukua muda gani hadi kufika hapo?"


"Ni nusu saa tena kwa kuwa njia ni ngumu sana na imejaa mchanga mwingi lakini pia kuna maeneo ambayo hayapitiki hivyo itatulazimu kutumia muda mwingi kuibua njia zenye kupitika kwa urahisi."


"Ok, na tufanye hivyo maana hapa tukijitokeza tu tumeharibu na tutaifanya kazi hii kuwa ngumu!" Alijibu kamanda Hamidu Jumbe.




Safari ngumu ikaanza tena huku wakiwa makini kutazama saa ili waweze kuendana na muda husika. Isingekuwa rahisi kutumia au kuendana na muda ule waliowekeana na kikundi chao cha ukombozi ikiwa hali halisi ya njia ni kama ilivyo. Njia ilikuwa ngumu na iliyojaa mchanga mwingi lakini pia kuna mahali iliwabidi kutambaa kama nyoka ili kuweza kujificha wasionwe na maadui zao ambao wako makini zaidi. Walipishana na nyoka wakali na wengine ikibidi kuwauwa. Hakukuwa na jinsi nyongine zaidi ya kufanya hivyo. Walitumia muda wa dakika thelathini na tatu hadi kufika mahali kusudifu. Ulinzi wa upande huo ulikuwa mwepesi sana kwani hakukuwa na mlinzi hata mmoja aliyekuwa akionekana kukatiza eneo hilo. Hamidu Jumbe akakamata darubini na kuiweka machoni tena ili kujihakikishia usalama, hakika kulikuwa tulivu na kusikoleta shaka ya aina yoyote. Walitoka hapo mbio wakiwa wameinama huku wakijikinga kwenye miinuko ya vichanga hivi na vile kuweza kujificha silaha zao makini walizozifunga sauti zikiwa macho mbele kwa lolote. Walibakisha hatua chache kuweza kuikabili nyumba hiyo. Mara akatokea mlinzi mmoja akiwa na mtutu wa bunduki. Alikuwa mrefu aliyevaa gwanda za jeshi la wanamgambo. Alikuwa amevimba shavu moja akitafuna mirungi huku akiendelea kuvuta sigara yake taratibu. Macho yake makali makubwa yaliyo na wekundu yalibebwa na sura kavu nyembamba na ndefu yenye alama moja ya kovu la kukatwa na kitu chenye ncha kali shavuni. Buti kubwa la kijeshi lilikuwa limemkaa vizuri miguuni mwake, hakuacha kutembea kwa kuweka vituo kila wakati ili kuhakikisha ulinzi wa eneo hilo.




"Nadhani kuko salama kila upande, unasemaje kamanda?" Aliuliza kamanda Rhoda akiwa amemuweka yule mwanajeshi mlinzi kwenye shabaha yake.




"Move left side mimi nitakava right side faster and clear." Alieleza kamanda Hamidu Jumbe huku akiruhusu rusasi yake ipenye kwenye shingo ya yule mlinzi. Walitoka kwa kasi eneo lile kisha ghafula wakajitupa chini kabla hata hawajafika kwenye sehemu walizopangiana. Macho yao yalimshuhudia mtu mmoja mrefu mwenye mwili wa saizi ya kati aliyevaa buti la ngozi la rangi ya kahawia na surualia nyeusi ya jeans sambamba na fulana nyueusi pia. Machoni akiwa hajavaa miwani hata hivyo hakuacha kuvaa kofia ya chepeo/kapelo ya rangi ya kibuluu iliyoyaonesha macho yake kwa uchache. Alikuwa yuko na mwendo wa kasi sana na matumatu akiwa makini kuanzia mwendo hadi utazamaji wake. Mikononi alikuwa amevaa glovu nyeusi na ngumu. Macho ya makomandoo hawa yalimtazama huyu mtu kwa umakini sana na utazamaji wao uliwatanabaishia kuwa mtu huyo hakuwa wa kawaida hata kidogo. Alionekana kuwa ni mwenye mafunzo ya daraja la juu la jeshi na aliyefuzu kwenye nyanja hizo za mapigano. Kamanda Hamidu Jumbe aliitoa kamera yake ndogo yenye nguvu na kupiga picha kadhaa kisha akairudisha mfukono mara baada ya mtu yule kupotelea garini upande wa dereva na kutoweka. Walitazamana kwa mara nyingine makomandoo hao kisha wakaoneshana ishara ya kusonga mbele. Walikimbia kama awali kisha kamanda Hamidu akaelekea upande ule wa kuume na kamanda Rhoda akachukua uelekeo wa upande ule wa kushoto. Hamidu Jumbe alichokifanya kwa haraka ni kuuvutia pembeni ule mwili wa yule mlinzi kisha kuuficha. Baada ya hapo akawa na kazi ya kupambana na walinzi wa upande aliyopo kimya kimya hadi kukutana na mwenzake kwa upande wa mbele. Halikuwa zoezi gumu sana kwa kuwa hilo lilikuwa ni shambulio la kushtukiza. Muda mfupi mbele wakawa wamekutana upande wa mbele huku wakiwa wamefanikiwa kulaza chini walinzi sita wa nje. Walizama kwa umakini mkubwa sana kwa upande wa ndani na walikuwa wakipita chumba hiki na kile. Milango yote ilikuwa wazi haikuwa imefugwa zaidi ya kurudishiwa tu. Walisukuma milango yote huku kila mmoja akiwa ni mlinzi kwa mwenzake. Wakati wakiwa wanaingia mlango wa tano kati ya milango sita ya jengo hilo, waligundulika baada ya mlango huo kuwa ni wenye kupiga kelele kutokana na bawaba zake kuwa kavu zisizo na kialainishi chochote. Risasi zikaanza kurindima huku kelele za kuamshana zikisikika hata hivyo waliwadondosha walinzi hao wawili kwa muda mfupi sana kwani kamanda Rhoda alikuwa ni mwepesi na mwenye shabaha kali. Wakati wale walinzi wakiwa wanapiga risasi hovyo, kamanda huyo wa kike alikuwa akitazama risasi zinapotokea akiwa amejitenga kwenye chumba kingine huku kamanda Hamidu akiwa ndiye mwenye kushambulia akiwa upande mwingine. Hii ilikuwa ni kazi nyepesi kuweza kuwasambaratisha kwa risasi zake kwa kuwa hawakuwa wakijua idadi ya wavamizi kwenye lindo lao. Kimya kilitulia kwa muda mfupi nao walipojihakikishia utulivu ndipo walisonga mbele hadi kuzama ndani ya chumba hicho kwa tahadhari kubwa. Purukushani kubwa ilikuwa ikisikika kwenye chumba ambacho kilikuwa kimehifadhiwa wajumbe wale wa kijeshi.




Wakaingia kwa tahadhari kubwa huku hofu ikiwa miilini mwao. Waliusukuma mlango taratibu hadi ulipopatikana upenyo. Ghafula Panya mkubwa alitoka mule ndani na kupita katikati ya miguu yao akikimbia hovyo. Walipumua kwa nguvu sana kisha wakautafuta tena utulivu na kuzama ndani. Kimya kilikuwa kikubwa sana. Miili miwili iliyosheheni majeraha mabaya ya kuchimbwa kwa silaha za ncha kali ikiwa imelala tuli sakafuni. Viti viwili ambavyo vilionesha kuwa ndivyo vilikuwa vikalio vyao wakati wa mateso hayo makali vilikuwa vimesimama vikiwa vitupu. Walijaribu kuwasogelea wale maafisa wakubwa jeshini ili kuona kama walibakiwa na uhai hata hivyo matuamaini hayakuwepo baada ya tundu moja dogo la risasi kwa kila mwili kuonekana kwenye paji la uso.




"Tumechelewa kamanda na muuaji tumemuacha amekwenda...!" Alizungumza kamanda Rhoda akiwa kwenye masikitiko makubwa.




"Inamaana tume...!" Hakumaliza kile alichokuwa anataka kuzungumza kamanda Hamidu mara baada ya kuona kitu cha hatari sana kwenye mwili wa mmoja wa mjumbe aliyekuwa amelala pale chini.








"Tumechelewa kamanda na muuaji tumemuacha amekwenda...!" Alizungumza kamanda Rhoda akiwa kwenye masikitiko makubwa.




"Inamaana tume...!" Hakumaliza kile alichokuwa anataka kuzungumza kamanda Hamidu mara baada ya kuona kitu cha hatari sana kwenye mwili wa mmoja wa mjumbe aliyekuwa amelala pale chini. Ubavuni mwa mjumbe yule kulikuwa na bomu kubwa la masaa ambalo kwa muonekano wa macho makali ya kamanda Hamidu, zilisalia sekunde tatu tu bomu lile kuweza kulipuka.




"BOOOM...!" Alipiga yowe huku wakitoka pale mlangoni na kukimbilia nje kisha kabla hawajafika mbali wakajirusha hewani sambamba na mlipuko mkubwa sana wa bomu lile. Jengo lile lilichanguka changu! Likasambaratika kabisa huku eneo lile likitifuka tifu! Kwa kutokana na uzito wa bomu lile. Moto mkali ukaibuka na kimya kikuu kikiwa kimelikumba eneo lile biwi kubwa la moto likiwa linaendelea kuwaka. Haikujulikana wanajeshi wale walikuwa upande gani na walikuwa hai ama la! Kimya!




Baada ya dakika ishirini na tano helkopta maalumu ya kijeshi ikatua eneo hilo na wanajeshi wane wakishuka. Walilikuta eneo lote likiwa kimya halina hata kelele zaidi ya sauti za moto pekee ambao ulikuwa ukimalizia kuliteketeza jengo hilo.




"Tazama pale naona watu wakiwa wamelala...!" Sauti ya kiongozi wa msafara ule ilisikika ikitoa maelekezo baada ya tafuta tafuta kubwa ya hapa na pale na kufanikiwa kuiona miili miwili ikiwa imelala tuli mchangani. Wanajeshi wale wane wakasogea eneo waliloelekezwa wakiwa na machela huku wanajeshi wengine wane wakiwa wameweka ulinzi kuizunguka ile Helkopta. Waliikuta miili miwili ikiwa imelala kimya. Akasogea mtaalamu wa afya kwenye kila mwili na kutazama kama miili hiyo ilibakiwa na uhai.




"Bado makamanda wetu wanapumua; wako hai!" Aliongea mtaalamu wa afya kisha wakaweka machela chini na kuipandisha ile miili ya kamanda Hamidu na kamanda Rhoda. Makamanda wale wawili walijeruhiwa vibaya sana kutokana na nguvu ya ule mlipuko ambao walichelewa kuwa mbali nao. Walionekana kuvuja damu kwenye kila upande wa miili yao.




"Dokta, anzeni kuwapa huduma ya kwanza...wamepoteza fahamu na hali zao ni mbaya sana, tunakwenda mashariki mwa mji huu kutokea hapa hadi ilipopigwa simu kwa mara ya kwanza na makamanda wetu hapo tutaikuta miili mingine ambayo maelekezo yake tuipewa tayari. Alisema mwanajeshi mmoja kiongozi wa ule msafara. Helkopta ile ikanyanyuliwa juu huku wanajeshi wawili wakiwa wananing'inia huku na huku kutazama usalama wa eneo lile au kutazama kama kuna viumbe wengine wangeweza kuwapata wakiwa hai wawe ni maadui au wa upande wao. Pamoja na kutumi darubini kali hata hivyo hawakuona chochote kila mahali kulikuwa kimya kabisa. Walikuwa wametafuta vya kutosha hata hivyo miili ya wajumbe wawili hawakuiona kabisa machoni mwao na waliyotakiwa kutoa taarifa kuhusiana na miili hiyo walikuwa katika hali mbaya mno kulikuwa hakuna namna zaidi ya kuondoka eneo lile kwani hatari ingeweza kutokea muda wowote na kusababisha makubwa yasiyotarajiwa.




Sasa ndani ya Helkopta ile kulikuwamo na jumla ya miili minne, miwili ikiwa ni ya maiti zile za wanajeshi waliotumwa kwenye hiyo operesheni ambao ni meja Deus na meja Ong'ong'o huku miili miwili ikiwa ni ya makomandoo walio mahututi huku imani ya kuwa wamepoteza wanajeshi muhimu kwenye ule mlipuko ikiwa juu sana. Helkopta ile ikapotelea angani ikilitafuta anga la Kenyatta.




________




Mvua kubwa ilikuwa ikinyesha jijini Dar es salaam, ilikuwa imeshatimu saa sita na dakika arobaini za usiku; saa saba kasoro dakika ishirini. Muda huu mishemishe za watu wengi zilikuwa zikiendelea ndani ya jiji hilo kama ilivyo ada ya wakazi wengi wa jiji hilo japo si kwa mazoea ya siku zote. Uwepo wa mvua hiyo kubwa ulisabisha utulivu kiasi fulani kwa kuwa baadhi ya watu waliuwa harakati zao za kiutafutaji nyakati hizo za usiku na kwenda kutafuta pumziko ingawa si wote. Magari machache yalionekana yakikatiza mitaa hii na ile huku mengine yakiegeshwa kwenye majengo kadhaa na nyingine zikiweka kambi kwenye maegesho ya magari ya mahoteli maarufu jijini hapo na kwenye mabaa ama kumbi za starehe. Jiji lilipendeza kwa kulitazama ndani ya usiku huo mkubwa. Wakati hayo yakiwa yanaendelea, utulivu ulikuwa mkubwa ndani ya Hoteli moja iliyopo barabara ya Afrikana. White Sands Hotel and The Beach Resort. Chumba kimoja cha hoteli hiyo kwenye ghorofa ya tatu, alikuwapo mzee mmoja akiwa kwenye utulivu mkubwa na mbele yake kulikuwa na tarakilishi akiwa anafuatilia jambo fulani kwa umakini mkubwa. Hakuonekana kuwa na papara katika utazamaji wake ama kile alichokuwa akikifuatilia, pembeni ya tarakilishi kulikuwa na bilauri iliyosheheni kinywaji laini akiwa anashushia taratibu. Muda mfupi baada ya kufuatilia kile alichokuwa akikifuatilia, punde akaachana na tarakilishi na kugeukia upande mwingine ambako kulikuwa na bahasha moja ya khaki ikiwa imefungwa kwa gundi kabisa. Akaichana ile bahasha kisha akachomoa karatasi mbili kutoka bahashani akaendelea kujipa utulivu katika kufuatilia kwa umakini na utaratibu mkubwa. Hakuwa mwingine huyu mzee, alikuwa ni mwalimu Daniel Matia Okale almaarufu mwalimu Dao. Hii ilikuwa ni siku ya tatu tangu alipoitwa kwenye kikao kizito ambacho kiliwakutanisha maafisa usalama mbalimbali wa ngazi za juu wakijadili jambo zito ambalo lilitokea wiki mbili nyuma. Kikao hicho kilikuwa kimekwenda kuzungumzia mustakabali wa yale yaliyokuwa yamefanywa na magaidi wa Somalia. Kwanini mwalimu Dao mkuu wa kitengo cha siri cha kijasusi na muhimu nchini ameitwa kwenye mkutano huo ambao ndani yake kulikuwapo na maafisa mbalimbali wa jeshi nchini...?




Ipo sababu na sababu hii haikuwa sababu ndogo na ikapelekea hata yeye kuwapo kwenye mkutano huo muhimu na mkubwa wenye kufikia maamuzi mazito. Ni baada ya mwili wa aliyekuwa na cheo cha Luteni usu Makame Daud kufikishwa kwenye Hospitali ya jeshi ya Lugalo jijini Dar es salaam. Uchunguzi wa haraka wa kijeshi uliofanywa na madaktari wa jeshi ndiwo uliosababisha hofu na kusitishwa kwa mazishi ya mapema ya mwili huo ambao ulipangwa kuzikwa kijijini kwao huko kwenye mji mdogo wa Bagamoyo. Madaktari wale wa kijeshi waligundua vitu viwili vyenye kukanganya sana, kwanza ilikuwa ni namna mtu huyo alivyouawa. Pili ikiwa ni utata wa kujua nini kilichochukua uhai wake.


Kivipi...?




Mwili huu ulikutwa na matundu mawili ya risasi moja likiwa lipo kwenye paji lake la uso na jingine likiwa shingoni ambalo liliivunja kabisa mifupa ya shingo yake. Huwenda labda hii ndiyo iliyoondoa uhai wa mwanajeshi huyu? Inaweza ikawa lakini pia kitu cha kuajabisha ni kwamba mwili huu ulikutwa na sumu za aina mbili, ya kwanza ikiwa ni ya kulevya ambayo muhanga akiinusa hulewa na kupoteza fahamu kabisa. Sumu ya pili ikiwa ni sumu mbaya ya kuuwa. Hii iliwachanganya hawa madaktari kwa kiasi kikubwa sana hadi kufikia hatua ya kutoa taarifa kwenye uongozi wa kijeshi mbali na ripoti ya kiuchunguzi waliyoiandaa. Kabla hata hawajaruhusiwa kuendelea na uchunguzi huo ilibidi hali hiyo iripotiwe kwenye vyombo muhimu vya kiusalama. Ndipo amuzi likatolewa kuwa madaktari bingwa na aminiwa wahusishwe kwenye kuongoza uchunguzi huo, majina ya madaktari wawili yakaorodheshwa kuingia kwenye uchunguzi huo. Daktari Lumoso Papi Mmbai ambaye aliaza kazi rasmi mara baada ya kuwa mapumzikoni kwa takribani miezi miwili alipotoka kwenye misukosuko kisha kuingizwa moja kwa moja kwenye kitengo cha kiusalama akiwa sambamba na dokta Limo Lihula. Uchunguzi huo ukafanyika kwa umakini mkubwa na kugundulika vitu vingi vya ajabu mwilini mwa mwanajeshi huyo.




Ripoti ya kiuchunguzi ilipotoka ndipo ikapelekea kuitwa kwa kiongozi wa kitengo hatari cha kijasusi nchini mwalimu Daniel Matia Okale, p.a.k mwl. Dao. Kikao kizito kikafanyika ambacho kilijumuisha mambo mengi huku ripoti maalumu ikimfikia Amiri jeshi mkuu ambaye alitoa amuzi kuwa baada ya hitimisho la kikao hicho apelekewe mrejesho wenye maazimio ya kueleweka. Kikao hicho kilizungumzia mambo mengi sana ikiwemo ulinzi na usalama wa mipaka ya taifa hili, usalama wa raia wake na ikiwa wao ni mioyo ya ulinzi wa kila kitu ndani ya taifani na mwisho ni namna watakavyoweza kufanya. Yaliibuliwa mengine ambayo yalikuwa yamepewa kisogo na yakatumika kama chanzo cha haya yaliyotokea. Ikahisika kuwa huwenda kilichokuwa kikisubiriwa ni sababu tu pekee lakini watendi wa jambo hilo wanayo dhamira ya kufanya hilo. Mkasa ule wa kuogofya ulitokea kijiji cha Kibatini pembezoni mwa mapango ya Amboni ukaibuliwa upya na maafisa hawa wa ngazi ya juu kabisa ya kiusalama. Wakachanganua namna raia wa vijiji vilivyozunguuka mapango yale ya Amboni walivyochinjwa kama kuku huku watendi wa tukio hilo la ajabu wakiyatumia mapango yale kama ngao yao ya kujifichia huku wakileta upinzani mkubwa na askari ambapo ilibidi kutumike nguvu kubwa kuweza kuwasambaratisha. Uzito wa mijadala hii ikapelekea kuchukuliwa kwa muda mwingi wa kikao hiki kizito kilichowaacha maafisa hawa katika hali ngumu ya kimaamuzi.




_______




Mwalimu Dao alijinyanyua kitini ndani ya chumba kile alimokuwa amejituliza akipitia zile karatasi ambazo ndizo zilizokuwa zimebeba uchunguzi wote huku maamuzi mazito akiwa amekabidhiwa yeye na kitengo chake. Kwa muonekano tu wa namna alivyojinyanyua kutokea kitini, ilidhihirisha wazi kuwa alikuwa amechoka sana. Macho yake yalikuwa mekundu kwa ukosefu wa usingizi kwa siku kadhaa, mwili wake alikuwa akiusukuma kwa kuulazimisha kwa namna ambavyo alichoka kimwili na kiakili.




"...ripoti ya madaktari wetu inasema kwamba mwili wa Luteni usu Makame Daudi umekutwa na alama tatu za kusababisha au kupelekea mtu kukumbwa na mauti; alikutwa na matundu mawili ya risasi, sumu yenye kulevya na kupotezesha fahamu, sumu hatari ya kuua aina ya VX Nerve Agent na alama tatu za kucha za mnyama jamii ya paka...!" Alikumbuka maneno haya yaliyokuwa yakitolewa na msomaji maalumu wa ripoti ile ya kidaktari mbele ya jopo zima la maafisa wa usalama nchini. Kumbukumbu hii ilimuumiza sana kichwa mwalimu Dao. Aliikita mikono yake juu ya meza na kuinama akiitazama ile ripoti kwa macho tulivu kama kwamba ni mara ya kwanza alikuwa akiipitishia macho. Hali ilikuwa ngumu sana.


VX Nerve Agent. Hii ni sumu hatari sana ambayo huuwa kwa haraka kuliko kawaida mara tu baada ya kuigusa ngozi ya mhanga. Na inaelezwa kuwa ujazo wa gramu 0.01 ya kemikali hii ambayo ni ndogo zaidi ya tone moja la kawaida, idondokapo kwenye ngozi inakuuwa kwa kuharibu mfumo mzima wa neva mwilini. Kitu kilichopelekea huyu mzee kuingia kwenye tafakuri nzito ni namna ambavyo kifo hiki kilikuwa tata. Baada ya kuwaza hicho akawaza risasi yaani matundu mawili ya risasi yaliyobakia kwenye mwili wa Makame Daudi. Risasi sumu, sumu risasi. Akawaza na kuwazua hata hivyo bado kichwa chake kilikuwa kizito mno kumfunulia majibu yaliyo ya kweli.




Mwalimu Daniel Matia Okale aliitazama saa yake ya mkono vilevile akiwa ameikita mikono yake mezani akiwa ameinama kisha akayahamisha macho yake kuitazama saa ya ukutani iliyopamba chumba kile. Akakuta sekunde ya mwisho ikiwa inadondoka na kubadili majira mazima, sasa ikiwa si saa saba tena bali ni saa nane usiku. Usiku wa manane ulitimia akiwa macho kodo.








Mwalimu Daniel Matia Okale aliitazama saa yake ya mkono vilevile akiwa ameikita mikono yake mezani akiwa ameinama kisha akayahamisha macho yake kuitazama saa ya ukutani iliyopamba chumba kile. Akakuta sekunde ya mwisho ikiwa inadondoka na kubadili majira mazima, sasa ikiwa si saa saba tena bali ni saa nane usiku. Usiku wa manane ulitimia akiwa macho kodo. Akashusha mzigo mzito wa hewa toka ndani ya mapafu yake kisha akasimama wima na kutoa pakiti ya sigara toka kwenye moja ya mfuko wake wa suruali na kuivuta sigara moja toka paktini na kuipachika kinywani mwake akatoa na kiberiti cha gesi akaiwasha. Aliivuta sigara ile kwa hasira sana kwa dakika moja kisha akaibana kwenye pacha ya vidole vyake na kuzirusha hatua zake taratibu hadi dirishani. Alilifunua pazia jepesi la dirisha na kulisogeza pembeni kisha akasogeza kioo na kuyaruhusu macho yake yalitazame jiji katika nyakati zile za usiku. Sasa akafanikiwa kujua kuwa kulikuwa na mvua kubwa ambayo ilikuwa ikiendelea kunyesha kwa fujo kubwa. Hakukuwa hata na mtu mmoja kwa majira yale zaidi ya gari chache ambazo zilikuwa zikikatiza kwenye barabara hii na ile. Macho yake yalikuwa makini kutazama hatua kwa hatua hata hivyo hakukuwa na kitu chochote ambacho aliweza kukiona kwa ufasaha maana akili yake bado ilikuwa na jazanda zito juu ya mkutano ule. Akiwa pale hakuacha kufikiria namna ambavyo atakavyoweza kufanya. Akiwa katika tafakuri ile huku akiendelea kuyachoma mapafu yake kwa ile sigara, alikuwa akiingia kwenye uchaguzi mkubwa wa kuamua kati ya vijana wake ni yupi alikuwa anafaa kuingia kwenye kazi ile ya kutisha namna ile. Vijana wake watatu walikuwa tayari wameshamaliza mafunzo yao japo wote walikuwa wako kwenye nchi tofauti wakiwa katika kufurahia likizo zao ambazo kitengo ilitoa kama hongera ya kumaliza mafunzo salama na kwa weledi wa hali ya juu huku wakiacha alama muhimu sana kwenye nchi ambazo walikuwa wakipokea mafunzo hayo. Alikuwa akiangalia nani kati ya hawa watatu ambaye angeweza kumpa jukumu hilo. Hakuweza kumhusisha Rajabu Omairy Isihaq, p.a.k Roi wala Catherine wa Catherine, p.a.k green bird kwakuwa kila mmoja alikuwa na sababu zake. Roi alikuwa bado yupo nchini Uganda akiwa na jukumu zito la kuhitimisha huku Catherine akiwa hana muda mrefu tangu amalizane na majasusi nchini Ungamo. Mtu wa kwanza aliyekuwa akimuweka kwenye nafasi kubwa alikuwa ni Iddiallan Simion. Huyu rekodi yake ilimridhisha sana na kila akiipitia kuisoma ilikuwa ikimpa faraja kubwa mno, si kama Happy hakuwa na rekodi nzuri lah! Bali kazi iliyoko mbele yake haikumhita mtu mwenye hasira za kupitiliza bali ilimhitaji mtu mwenye kutafakari kwa kina na mwenye kuvuta subira. Happy sifa hizi hakuwa nazo japo alikuwa hatari na mbishi asiyekubali kurudi nyuma ila alipenda kumuacha kwanza hadi itakapobidi kufanya hivyo. Hawa watu wawili ndiyo aliyokuwa akiwafikiria sana na amuzi lake likaishia kwa Iddy na si vinginevyo, Happy na Moniela akiwaacha kwanza waendelee na likizo zao fupi. Alitoka pale dirishani baada ya kukitupia kile kipisi cha sigara nje akarudi moja kwa moja pale kwenye meza na kuaza kuandika hiki na kile kwenye tarakilishi yake huku akituma baadhi picha na kadhalika kisha akapunguza nguo zake baada ya kuizima tarakilishi ile na kuelekea maliwatoni. Alikuja kulala saa tisa na dakika ishirini na tano usiku.




_______




LONDON; UINGEREZA.




Barabara ya Peckam ambapo ilipandwa Best Western London Peckam Hotel, palikuwa na uchangamfu mkubwa kiasi huku gari nyingi za daraja la kati zikiegeshwa kwenye magesho ya magari ya Hoteli hiyo ya nyota nne. Miongoni mwa gari hizo ambazo zilikuwa zikiegeshwa maegeshoni hapo, ilikuwapo gari moja aina ya Mercedes benz Vito Van ya rangi ya kibuluu mali ya Hoteli hiyo. Baada ya gari hiyo kuegeshwa maegeshoni hapo, mlango wa mbele wa upande wa dereva ulifunguliwa akashuka kijana mmoja mrefu kiasi mwenye mwili wa wastani ulioshiba mazoezi ya mara kwa mara. Alivaa fulana ya mirabamiraba ya rangi nyeupe na mawingumawingu, suruali ya jeans ya rangi ya kibuluu iliyowiva na raba nyeupe zilizomkaa vema miguuni. Alivutia kumtazama kwa rangi yake ya chokoleti kijana huyo wa ki-Afrika. Alilitazama lile eneo kwa namna ya kumvutia kisha akalitazama lile gari ambalo ni wiki sasa limekuwa chini ya himaya yake baada ya kulikodi kutoka hotelini hapo kwa minajili ya kuweza kulitumia katika mizunguuko yake ya kawaida ya kila siku. Hatua zake za taratibu zilimfikisha ndani ya hoteli ile eneo la mapokezi ambapo aliwakuta wasichana wawili wa kizungu akawasabahi kwa tabasamu mwanana huku wasichana hao wakirudisha salamu hiyo kwa namna ileile. Walionekana kuzoeana kiasi fulani labda ni kutokana na ukaaji wake wa muda sasa tangu kuingia jijini hapo na kuchukua chumba ndani ya Hoteli hiyo. Walichekeana na kufurahi huku akimvuta msichana mmoja miongoni mwa wale wawili na kumpiga busu moja kali sana la shingoni kisha kumuachia na kukimbilia mahali ngazi za kulikwea jengo lile refu zilipo. Hakutaka kutumia lifti kutokana na kuwa hakuwa amechukua chumba mbali sana. Hali ile ilimfanga yule msichana kumfukuza, sasa wakawa wanazikwea ngazi pamoja hadi walipofika ghorofa ya tatu kwenye korido ndefu na nyembamba ya kuvutia ambayo ilikuwa na mwanga hafifu wa taa zilizokuwa zikiifanya kazi yake vema ya kupendezesha eneo hilo. Hii korido ilikuwa imetenganisha vyumba vingi huku na huku. Hapa yule msichana alimrukia yule kijana na kumpandia mgongoni kisha kuikunja miguu yake kiasi kumfanya abembee kwenye mgongo wa kijana yule.




"Jabir umekuja wakati muafaka sana maana ni muda huu mwenzangu ameingia na kunipokea zamu, nimekukumbuka sana mpenzi wangu hivyo ni muda mzuri wa kufurahi tukiwa pamoja hadi saa kumi na mbili za jioni ambapo utanisindikiza nyumbani, nataka kwenda kukupikia chakula kizuri leo na kukuogesha kisha tunarudi tena kitandani kwa mara nyingine ukiwa kwangu. Sichoki kufanya mapenzi nawe Jabir wangu kwa kuwa ni mtu mtundu sana na una manjonjo mengi kiasi kwamba najiona ni mwanafunzi kila wakati niwapo kitandani nawe. African boy you kill me!" Aliongea mengi yule msichana huku akiwa bado anabembea kwenye mgongo wa kijana aliyemtambulisha kwa jina la Jabir. Jabir hakujibu kitu yeye alizidi kuzirusha hatua zake za taratibu kama ambaye hakuwa akimsikia msichana huyo.




"Au unataka tutoke nje ya hapa, tukaogelee kwenye mabwa mazuri ya kuogelea tukiwa wenyewe na kufurahia maji huku tupeana penzi la majini, au unataka twende sehemu tulivu na kuimaliza siku hii kwa kufanya mapenzi...? Vyovyote vile utakavyo mpenzi wangu niko tayari hata ukitaka tuhamie Hoteli nyingine ni sawa tu ilimradi nisilikose penzi lako kabisa siku ya leo maana nahisi kuchanganyikiwa kwa kulikumbuka." Alizidi kubwabwaja huku Jabir akionekana kuendelea kupiga hatua pasipo kumjibu. Binti huyo alipatwa na mashaka sana kwa kutokujibiwa hivyo akaamua kumuita ili kujua kama kati ya alivyoongea kuna jambo haliko sawa na lilimkera Jabir. Pamoja na kuita hata hivyo hakujibiwa na Jabir aliendelea kupiga hatua tu. Punde msichana yule alijikuta akigeuzwa juujuu na kupinduliwa kisha kusukumwa nyuma nyuma taratiibu bila hofu huku Jabir akionekana kuwa mkavu wa sura kupita kiasi. Yule msichana akahisi labda yule siye Jabir anayemfahamu maana pamoja na utaratibu ule, ile haikuwa kawaida ya mpenzi wake. Alimsimamisha kwenye mlango wa chumba namba 105 kisha akawa anamtazama kwa namna ya kumchunguza sana.



ITAENDELEA


imulizi : Mikono Ya Jasusi 


Sehemu Ya Pili (2)




Hofu ikazidi kuibuka kiasi akaanza kuhisi hatari.




"Vile upendavyo mpenzi maana kwa jinsi nilivyolikumbuka penzi lako naona kama vile muda uliousema hautanitosha...!" Sauti nzito ya Jabir iliyojaa mahaba mazito iliingia moja kwa moja kwenye masikio ya yule binti na kumfanya alegee miguu kisha pumzi nzito kumshuka. Kijana yule alikuwa akizungumza huku akipitisha kadi maalumu ya kufungulia mlango na mlango ulipofunguka yule msichana alimsukuma Jabir nyuma na yeye akaingia ndani kama aliyechukizwa na kitendo kile cha kutishwa. Jabir alisimama kwa sekunde kadhaa kisha akaingia kwa haraka na kumbeba mpenzi wake juu kisha akamtupia kitandani, alijitupa naye wakaanza kugalagazana pale kitandani kwa muda mwingi huku wakitomasana hapa na pale hadi walipotulia yule msichana akiwa chini na Jabir juu. Jabir alipokea kofi moja jepesi lililotua shavuni.




"Sijakuzoea hivyo Jabir wangu mbona umeamua kuniweka roho juu sasa...?" Aliuliza yule msichana kwa sauti tamu iliyozidiwa na mahaba mazito.




"Kuna wakati masikhara huanzia mbali Cecy mpenzi, huoni kuwa nimekujua ukiwa katika hofu unakuaje...!" Alijibu Jabir katika hali ya utani.




"Sitaki hukoo...muone kwanza...Aaagh...!" Alilalama hata hivyo hakumaliza malalamiko yake baada ya kutekenywa kwa kuguswa mbavu zake changa. (Mazungumzo haya yote yalitumia lugha safi ya kiingereza).




"Kofi ulilonipiga nitalilipa kwa bakora za kutosha nitakazokucharaza nazo." Aliongea Jabir huku akimpindua msichana huyo kumgeuza upande huu na ule.




"Niko taya...!" Alishindwa kuimaliza kauli yake Cecy mara baada ya sauti ya muito wa simu ya mule chumbani kuanza kuita kwa fujo nyingi. Cecy ilimkera sana hii simu kwa kuwa kwake ulikuwa ni muda muafaka wa kumkaribisha Jabir mwilini mwake. Mshangao wa sekunde tatu ukawafanya waitazame ile simu ambayo ilizidi kuita kwa fujo. Jabir akaruka kutokea pale kitandani kabla simu ile haijakoma kuita akanyanyua kiwambo cha simu na kuiweka sikioni na kusikiliza.




"Unayajua mawasiliano yetu ya mara kwa mara...!" Sauti nzito ilisikika masikioni mwake hii ikapelekea kuweka mkono kwenye kiwambo cha kutolea sauti na kuziba, hivi ni baada ya kuifahamu sauti ya mpigaji wa simu hiyo. Simu hiyo ilipigwa kutokea nje ya nchi na hiyo ni baada ya mpigaji huyo kuitambua Hoteli aliyofikia Jabir hivyo moja kwa moja alikwenda kwenye mtandao wa Hoteli hiyo na kupata mawasiliano ya moja kwa moja ambapo alipiga na kupokelewa na watu wa mapokezi ambao waliisikiliza shida yake kisha kumpa namba au maelekezo mtu huyo namna ya kuongea na mtu amtakaye akiwa chumbani kwake baada ya yeye kujieleza kwa kina.


ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog