Search This Blog

Saturday 24 December 2022

KILIO CHA MIFEREJI YA DAMU IENDAYO ETHIOPIA - 4

   http://pseudepigraphas.blogspot.com/2020/06/kilio-cha-mifereji-ya-damu-iendayo_10.html

Simulizi :  Kilio Cha Mifereji Ya Damu Iendayo Ethiopia

Sehemu Ya Nne (4)



Katika kipindi cha miezi mitatu ambayo RPF walikuwa kimya, serikali ya Rwanda walikuwa wamejiaminisha na kuamisha ulimwengu kwamba wamewashinda RPF. Kwa hiyo kama RPF walikuwa wanarejea tena kwenye uwanja wa vita walihitaji wafanye kitu ambacho watawadhalilisha serikali kwa kujipatia ushindi wa haraka. Lakini pia ushindi huo wa haraka utatoa taswira ya ufanisi wa hali ya juu ya vikosi vya RPF na hivyo kuanza kujenga hofu ndani ya wanajeshi wa serikali.


Kwa hiyo ili kujihakikishia ushindi mkubwa na wa haraka walihitaji sehemu ambayo wanaweza kuishmbulia kwa kushitukiza.

Sasa mji huu wa Ruhengeri uko kusini mwa milima ya Virunga. Yaani kwamba ukishuka milima ya Virunga haraka sana unakutana na mji huu. Kwa hiyo hii ilikuwa ni sehemi mujarabu kabisa kwa 'ambush'.


Lakini hii haikuwa sababu pekee… kulikuwa na sababu nyingine kubwa zaidi na ya kisaikolojia zaidi.



Rais Habyarimana pamoja na mkewe na familia yote ya mkewe ambayo ilikuwa na ushawishi mkubwa kama ambavyo nilieleza huko nyuma wanatokea eneo hili na ukanda huu. Kwa hiyo Wanyarwanda wengi kipindi hicho waliona eneo hili na ukanda huo kama ni 'moyo' wa nchi.

Ni kama vile ingekuwa hapa Tanzania tuseme kikundi chenye malengo hayo washambulie Chato na kanda ya ziwa, au miaka miwili nyuma tuseme wangeshambulia Msoga na eneo lote la Chalinze.


Kwa hiyo lengo lake kuu hapa lilikuwa ni moja kutoa ujumbe kwamba RPF ipo na iko na nguvu lakini pia pili ilikuwa ni kuleta taharuki ndani ya serikali.


Lakini pia kulikuwa na sababu nyingine ya tatu ya kwa nini walichagua mji huu. Na sababu hii ya tatu ilikuwa ni Gereza kuu la Ruhengeri. Nitaeleza sababu hii muda si mrefu.


Upande wa pili nimesema ni namna ambavyo walikuwa wanafanya mashambulizi.



Usiku wa January 22, 1991 wanajeshi mia saba wa RPF waliteremka kutoka kwenye milima ya Virunga mpaka chini kabisa karibu na mji na kujificha. Walisubiri mpaka asubuhi ya tarehe 23 January na kuuvamia mji.


Vikosi vya jeshi vya serikali vilichakazwa kama watoto wadogo. Auheni yao kidogo waliipata baada ya serikali ya Ufaranasa kwa haraka kupeleka wanajeshi wao pia kuongeza nguvu. Mwanzoni asubuhi hiyo waliwatunishia misuli RPF lakini mpaka kufika mchana tu, vikosi vya serikali ya Rwanda pamoja na wanajeshi wa Ufaranasa walikuwa wamepigwa kwa aibu kabisa.


Kwa hiyo mpaka kufikia mchana, RPF walikuwa wameuweka mji mzima wa Ruhengeri kwenye kiganja chao. Na ndipo hapa ambapo Kagame alianza kuitesa serikali kwa 'mind games' na kuonyesha ugwiji wake.


Nimeeleza kwamba sababubya tatu ya RPF kuchagua mji huu ilikuwa ni Gereza kuu la Ruhengeri.

Sasa baada ya mji mzima wa Ruhengeri kuwekwa chini ya RPF, Charles Uwihoreye Mkuu wa Gereza hili baada ya kufahamu kabisa kwamba hakukuwa na tumaini lolote la kulinda gereza lake dhidi ya wapiganaji wa RPF, alipiga simu Kigali makao makuu ya serikali ili kuomba maelekezo ni nini anatakiwa kufanya.


Serikali pasipo kusita au kufikiria mara mbili mbili walimuamuru ashirikiane na askari wenzake magereza wawapige risasi wafungwa wote.


Ikumbukwe kwamba gereza hili pia lilikuwa linamshikilia Bw. Théoneste Lizinde, ambaye zamani alikuwa swahiba mkubwa wa Rais Juvenile Habyarimana lakini baadae alifanya jaribio la kumpindua swahiba wake Rais Habyarimana.


Kagame alikuwa anamtaka mtu huyu akiwa hai. Lakini Mkuu wa Gereza alipewa amri awapige risasi wafungwa wote.


Itaendelea…




SEHEMU YA NANE




Kama ambavyo nilieleza kwenye sehemu iliyopita kwamba Kagame alichagua mji wa Ruhengeri kuwa mji wa kwanza kuushambulia kutokana na sababu tatu… kwanza ulikuwa ni mji wa Ukanda ambao anatoka Rais Habyarimana na mkewe, pili mji ulikuwa chini ya milima ya Virunga ambayo RPF walikuwa wameweka kambi kwa kipindi cha miezi mitatu lakini pia walichagua mji huu kutokana na uwepo wa Gereza kuu la Ruhengeri ambalo ndilo lilikuwa gereza kubwa kushinda magereza yote nchini Rwanda.


Mkuu wa Gereza mara ya kwanza alipiga simu Kigali na kuongea na Kanali Elie Sagatwa ambaye alikuwa ni moja ya wale 'akazu' ambao niliwaongolea huko nyuma (inner circle ya Rais Habyarimana ambayo ilijengwa na ndugu wa mkewe na familia yake).

Kanali Sagatwa alimuamurj kwamba ashirikiane na askari wenzake awapige risasi wafungwa wote.


Mkuu wa gereza Bw. Charles Uwihoreye kwa kiasi fulani kuna chembe za busara zilimjia kichwani… mji wote wa Ruhengeri ulikuwa chini ya RPF kwa hiyo hakukuwa na uwezekano wa wao kutoka mahala hapo na kukimbia salama. Kwa hiyo kama anahitaji kuishi ni vyema awe na kitu fulani cha kuwafurahissha RPF.


Uwihoreye alikataa kutekeleza agizo hilo la kanali Sagatwa la kuua wafungwa wote.

Ilibidi Sagatwa awasiliane na Rais Habyarimana kumueleza kuhusu kinachoendelea gereza la Ruhengeri. Rais Habyarimana akatoa ruhusa kwamba wafungwa wote wapigwe risasi.

Kanali Sagatwa akapiga simu tena kwenda kwa mkuu wa gereza Ruhengeri kumtaka atekeleze agizo hilo na kumsisitiza kwamba agizo limethibitishwa na amri kutoka kwa Rais.


Kwa mara nyingine tena Mkuu wa gereza alikataa katakata kutekeleza agizo hilo.

Dakika chache baadae wapiganaji wa RPF walivamia gereza la Ruhengeri na kuliweka mikononi mwao. Kutokana na kitendo cha mkuu wa gereza kuweka msimamo na kukataa kutekeleza agizo la Rais Habyarimana na kanali Sagatwa kuua wafungwa wote, RPF walimsamehe mkuu wa gereza na kumuacha aishi japokuwa isingekuwa hivyo ni lazima wangempiga risasi kutokana na mafungamano yake na Rais Habyarimana.


Wafungwa wote wa gereza la Ruhengeri waliachiwa huru huku Bw. Théoneste Lizinde ambaye alikuwa ni moja wa wafungwa kwenye gereza hilo na rafiki mkubwa wa zamani wa Rais Habayarimana kabla ya kumsaliti na kutaka kumpindua, alishawishiwa na kujiunga na RPF kutoka na taarifa adhimu ambazo alikuwa nazo kuhusu serikali nzima na Habyarimana mwenyewe binafsi.



Wapiganaji wa RPF waliushikilia mji mpaka mida ya alasiri kabla ya kuondoka na kurejea msituni kwenye milima ya Virunga. Tayari walikuwa wamefanikiwa kutuma ujumbe waliotaka kwamba, RPF bado iko na iko imara na pia walikuwa wamemdhalilisha Rais Habyarimana na kuonyesha udhaifu wa jeshi lake.


Ilipita siku moja nyinginendipo serikali ilitangaza hali ya hatari nchi nzima na kutuma vikosi vingine vya jeshi kwenda mji wa Ruhengeri.


Wapiganaji wa RPF waliendelea kuuvamia mji wa Ruhengeri kila siku usiku na kupambana na vikosi vya serikali. RPF hawakuwa na ya kuushikilia huu mji. Walikuwa wanafanya hivi (kuvamia usiku na kuondoka) ili kuwachosha tu vikosi vya serikali. Hii ni moja ya mbinu adhimu ya kisaikolojia ambayo kagame aliitumia sana kwenye vita. Kumchosha kwanza adui vya kutosha na kisha kufanta shambulio kubwa madhubuti.


Kwa hiyo hatimaye nchi ya Rwanda ikarejea vitani tena baada ya kutulia kwa karibia miezi minne.


b6de20020995ea1aaa39875dedc20e33.jpg


Vita iliendelea kupamba moto. Majeshi ya serikali yalizunguka sehemu zote muhimu za milima ya Virunga. Ubaya ni kwamba RPF ndio ambao walikuwa wako sehemu ya kimkakati (juu ya milima) kwa hiyo vikosi vya serikali walikuwa hawawezi kufanya "all out assault" kwenda juu mlimani.


Kagame aliendelea kuwaongoza wapiganaji wa RPF kufanya mashambulizi makali na kisha kurudi kujificha milimani. Walikuwa wanafanya hivi mara kwa mara na kwa umahiri mkubwa.

Kuna wakati kagame alikuwa anawaongoza wapiganaji wake kushambulia maeneo kumi tofauti kwa pamoja ili kuwachanganya vikosi vya serikali wasijue ni wapi hasa ambako walipaswa kuelekeza nguvu zao.


Mashambulizi ya namna hii yaliendelea kwa miezi kadhaa huku taratibu RPF wakipata kile ambacho walikuwa wanakitaka. Walifanikiwa kuwachosha vikosi vya serikali na hatimaye kuanza kuweka maeneo muhimu kwenye himaya yao. Moja ya maeneo ya kimkakati kabisa ambayo RPF walifanikiwa kuyaweka chini yao ilikuwa ni mji wa Gatuna ulioko mpakani.

Mji huu ndipo ambapo mizigo yote kutoka bandari ya Mombasa inapitia hapa na kuingia ndani ya Rwanda.

Hii iliifa ya serikali ya Rwanda kubadili route na kuanza kutumia bandari ya Dar es Salaam kwa kiwango kikubwa ambapo route hii gharama yake ni kubwa mno kulinganisha na gharama ya kutoka bandari ya Mombasa kuingilia mji wa Gatuna.


Kutokea hapa kwenye mji huu taratibu vikosi vya RPF vilianza kusonga mbele. Mpaka kufikia mwishoni mwa mwaka 1991 vikosi vya RPF vilikuwa vimeweka chini ya himaya yao karibia 5% ya nchi ya Rwanda.


Wakahamisha makao makuu yao kutoka kwenye milima ya Virunga mpaka jimbo la Byumba karibu na mji wa Mukindi ambako kulikuwa na kiwanda cha chai kilichotelekezwa kutokana na vita hiyo na wakafanya hizi kama ofisi zao na makao makuu yao.


Katika kipindi hiki ndipo ambapo Wahutu nao labda kwa kiasi fulani waliweza kuhisi yale maumivu ambayo Watusi waligapitia kwa miongo kadhaa ya kuishi kama wakimbizi. Miji mingi hii ambayo RPF waliiteka ilikuwa na idadi kubwa ya wakazi wa kabila la Kihutu. Kwa hiyo baada ya miji kutekwa na RPF ilibidi wakimbie miji hiyo, lakini hawakuweza kukimbilia Uganda kwa kuwa RPF walikuwa wanamiliki eneo kubwa la mpakani. Hivyo kwenye kipindi hiki Rwanda ilishuhudiwa ikiwa na idadi kubwa zaidi ya wakimbizi wa ndani (internally displaced).



Japokuwa kuibuka tena huku kwa vita kulikuwa na manufaa makubwa kwa RPF ambao walionekana kuchanja mbuga siku baada ya siku lakini kulikuwa na athari kubwa kwa watusi ambao walikuwa ndani ya Rwanda. Mateso yalianza tena upya kwa kiwango cha juj zaidi.


Kwanza yalianza kama tukio dogo tu... ambapo wafugaji wapatao 60 wa Kitusi katika wao pamoja na mifugo yao walikatwakatwa mapanga kwenye eneo la Kinigi. Baadae mauaji haya dhidi ya Watusi yalianza kuenea kuelekea mikoa ya kusini mpaka maeneo ya Ruhengeri na Gisenyi.

Ndani ya muda mchache tu Rwanda ilishuhudia mauajibya zaidi ya Watusi 1000. Mwezi June, 1991 vikosi vya RPF na vikosi vya serikali viliweka makubaliano kwamba pande zote mbili ziruhusu waathiriwa wa vita hiyo kukimbia na kwenda kujificha sehemu salama. Kwa kiasi fulani ilipunguza kasi ya raia wasio na hatia kuuwawa. Lakini rohonu bado kila pande ilikiwa imejawa na vihoro wakitaka kutimiza lengo ambalo walikuwa nalo mioyoni mwao.


d012bd6e78a37abce10efcd5d169f0e7.jpg

Agathe Habyarimana



Kwenye sehemu zilizopita huko nyuma nilieleza kidogo juu ya uwepo wa 'Akazu' mara baada ya Rais Juvenile Habyarimana kushika madaraka.

Nilieleza pia kuwa moja ya vitu muhimu ambavyo vilimsaidia Habyarimana kubaki madarakani ilikuwa ni ushawishi na nguvu ya familia ya mkewe Agathe Habyarimana. Sasa basi hawa 'Akazu' walikuwa ni ndugu wa Agthe Habyarimana pamoja na ndugu wachache wa Habyarinama mwenyewe na watu wake wa karibu. Watu hawa walikuwa wamejipa jikumu la kuamua hatma ya nchi ya Rwanda, kwamba hawataki uwepo wa Watusi kwenye 'nchi yao'.

Hivyo basi kikundi hiki ambacho kilikuwa na nguvu kubwa mno, kilikuwa kinaratibu matukio mengi ovu dhidi ya watusi.


Jina lingine ambalo walijipachika lilikuwa ni "Zero Network" wakimaamisha kwamba lengo lao kuu lilikuwa ni kuwa na Rwanda yenye idadi sifuri ya Watusi.


Akazu ndio ambao walichochea kuibuka kwa itikadi ya "Hutu Power". Itikadi ya msimamo mkali dhidi ya Watusi na hata Wahutu wenye kuwakumbatia Watusi. Akazu walikuwa na kikundi chao cha wapiganaji kilichoitwa 'Impuzamugambi' na miezi michache baadae walichangia pia kuratibu kuibuka kwa kikundi cha 'intarahamwe' ambavyo tutavijadili zaidi hapo mbele kidogo.


Akazu walianzisha propaganda ya hali ya juu dhidi ya Watusi. Walifika mbali mpaka kufungua vituo vya redio na kuchapisha majarida kueneza ujunbe wao wa propaganda.

Ujumbe wao ulikuwa ni mmoja tu, kwamba Watusi si Wanyarwanda na hawana haki ya kuwepo hapo.


Propaganda hizi zilienda mbali zaidi na kufikia hatua ya wanachama wa Akazu wenye nguzu wakiongozwa na mwanahabari nguli n mmiliki wa gazeti maarufu kipindi hicho lililoitwa 'Kangura' kukaa chini na kuyengeneza "AMRI KUMI ZA WAHUTU" ambazo walizichapa kwenye gazeti la Kangura na majarida yote yanayoendeshwa na Akazu.


Amri hizi kumi ulikuwa ni muongozo ambao Wahutu wote walikuwa wanapaswa kuufuata kuanzia muda huo katika maisha yao.


Amri zenyewe ni hizi;


1. Kila mhutu anapaswa kujua kwamba kila mwanamke wa Kitusi, haijalishi ni nani, anatetea maslahi ya Watusi wenzake.

Hivyo basi Mhutu yeyote atakayefanya yafuatayi tutamuhesabu ni msaliti:

- anaye muoa mwanamke wa Kitusi

- anafanaye urafiki na mwanamke wa Kitusi

- anayemuajiri mwanamke wa kitusi kama sekretari au muhudumu wa ndani


2. Kila Muhutu anapaswa kujua kwamba mabinti zetu wa Kihutu wanafaa zaidi na wenye kuwajibika kama wanawake, wake na mama wa familia. Je sio wazuri, kufaa kuwa masekretari na waaminifu zaidi?


3. Wanawake wa Kihutu muwe hodari, washaurini waume zenu na watoto wenu wa kiume wajielewe.


4. Kila Muhutu anapaswa kujua kwamba Watusi wote sio waaminifu kwenye biashara. Malengo yao pekee ni yeye na kabila lao kutawala. Hivyo basi Muhuti ambaye atafanya chochote kati ya hivi atahesabika ni msaliti;

- atakayefanya ubia wa kibiashara na Mtusi.

- atakayewekeza fedha zake au za serikali kwenye kampuni ya Mtusi.

- kukopa au kumkopesha Mtusi

- atakayefanya fadhila ya kibiashara kwa Mtusi (kupata kibali cha kuagiza bidhaa nje, mkopo wa benki, ujenzi, masoko ya umma n.k.)


5. Nyadhifa zote za kimkakati za kisiasa, kiutawala, kiuchumi, kijeshi na kiusalama zinapaswa kuaminiwa kwa Wahutu pekee.


6. Sekta ya elimu (wanafunzi na walimu) inatakiwa kujazwa na Watusi kwa idadi kubwa zaidi.


7. Wanajeshi wote wa Rwandan Armed Forces wanapaswa kuwa Wahutu. Vita ya mwaka 1990 imetupa somo. Na hakuna mwanajeshi ambaye anaruhusiwa kuoa Mtusi.


8. Wahutu wanatakiwa kuacha kuwaburumja Watusi.


9. Wahutu, popte walipo, wanatakiwa kuungana na kushikamana na kutafakari hatma ya ndugu zao wahutu

- Wahutu walio ndani na nje ya Rwanda lazima muda wote wawatunze ndugu zao wahutu.

- wanapaswa kupinga propaganda za Watusi bila woga.

- wahutu lazima wawe shupavu na wakali dhidi ya adui yetu Watusi.


10. Mapinduzi ya mwaka 1959, Mabadiliko ya katiba ya mwaka 1961 na itikadi ya Kihutu inapaswa kufundishwa kwa Wahutu wote katika ngazi zote.

Itikadi hii pia inapaswa kusambazwa kwa kasi na Muhutu popte ulipo. Mhutu yeyote mwenye kumkataza au kumsema Muhutu mwenzake kwa kusambaza itikadi hii atahesabika ni msaliti.




Amri hizi kumi zilisomwa kwenye vituo vya redio, kuchapwa kwenye magazeti na majarida na kusambazwa kwenye vipeperushi mitaani.

Itikadi ilienea kwa kasi kama moto wa kifuu.


Kagame kwa kuona hatari iliyo mbele naye alifungua kituo cha redio jijini kampala kilichoitwa Radio Muhabura kwa ajili ya kueneza propaganda za kupinga itikadi ya "Hutu power" na amri kumi.. lakini haikufua dafu.

Bundi alikuwa ametua mlangoni na hakukuwa na wakumfanya aruke kwenda mtini.


Harufu ya damu zaidi ilinukia.



3844d5c2070941e4a6bbfa8e997bbf93.gif

Kurasa ya mbele ya gazeti la Kangura tolea la November 1991... hayo maandishi makubwa ya kichwa cha habari tafsiri yake ni "Watusi: Wana wa Mungu"

Tamaza hayo maandishi pembeni ya picha ya Panga... maana yake "Silaga gani tutumie kuwaua hawa mende?"

Alafu pembeni hiyo picha kubwa ni Rais wa zamani Gregoire Kayibanda aliyeongoza mapinduzi na umwagaji damu wa mwaka 1959 na kuwafanya Wahutu kabila tawala.




Itaendelea...




SEHEMU YA TISA


428cc91675287bf3c9b5383fb8af5d56.jpg


Kwenye sehemu iliyopita nilieleza namna ambavyo Kagame aliwaongoza RPF kufanya mashambulizi ya akili dhidi ya vikosi vya serikali ya Rais Habyarimana.

Pia nilieleza namna ambavyo baada ya mashambulizi hayo yenye mafanikio ya RPF kuliibuka tena upya kwa kasi kubwa mauaji dhidi ya Watusi walioko ndani ya Rwanda. Baadae Wahutu wenye mamlaka na ushawishi wakaanzisha kampeni ya kuhamamisha uuaji wa watusi, kampeni ambayo iliendeshwa kwa propaganda kwenye radio na machapisho ya majarida, magazeti na vipeperushi.



Tuendelee….





MAJADILIANO YA AMANI JIJINI ARUSHA


Licha ya serikali ya Rais Habyarimana kuratibu propaganda hizi dhidi ya watusi lakini jumuiya ya kimataifa hasa, nchi ya Ufaransa ambayo wana maslahi ya moja kwa moja kwenye nchi ya Rwanda, kwamba jamii ya kimataifa walihitaji amani irejee tena ndani ya Rwanda.


Baada ya presha hii kuwa kubwa sana ilimbidi Rais Habyarimana kutangaza kwamba anaruhusu kurejea tena kwa mfumo wa vyama vingi.

Ufaransa waliamini kwamba kama demokrasia ingeruhusiwa tena na watu kupata majukwaa ya kusemea kero na madukuduku yao na kuwania uongozi wa nchi, basi labda mapambano ya silaha yangekoma.


Ni katika kipindi hiki Rwanda ilishuhudia kuanza kuundwa tena kwa vyama bya siasa kama vile Republican Democratic Movement (MDR), Social Democratic Party (PSD) na Liberal Party (PL).


Licha ya hatua hii muhimu iliyopigwa na nchi ya Rwanda kuruhusu demokrasia lakini ubaya ni kwamba Rais Juvenile Habyariamana rohoni mwake bado alikiwa na nia ovu. Moyoni mwake alikiwa amejawa na woga wa kupoteza madaraka yake. Kwa hiyo alichokuwa anakifanya ni kuweka mkono wake kwenye uanzishwaji wa vyama vyote hivi vya kisiasa. Yaani kwa maneno mengine vyama hivi vya siasa vilikiwa ni geresha tu ili kuridhisha jumuiya ya kimataifa.


Hii inathibitishwa na hata misimamo ya vyama hivi ambavyo vyote vilikuwa vinapinga vikali RPF na Kagame. Au ushahidi mwingine ni kuanzishwa kwa chama cha Coalition for the Defense of the Republic (CDR) ambacho kilianzishwa katikati ya miaka ya 1991. Chama hiki kilikuwa na msimo mkali wa kihutu na kukandamiza watusi kuzidi hata chama tawala cha Habyarimana mwenyewe, MRND. Na pia chama hiki kilikuwa na mafungamano makubwa na 'akazu'.


Rais Habyarimana ili kuwafurahisha jamii ya kimataifa kwa viini macho vyake, mwezi October 1991 aliunda upya baraza lake la mawaziri. Lakini baraza hilo ajabu halikujumuisha wanasiasa kutoka chama kingine chochote zaidi ya chama chake cha MNRD.

Hata wale ambao walikuwa wanajitahidi kuunda vyama vya kweli vya upinzani ambavyo havifungamani na Rais Habyarimana na genge lake, walikuwa wanapotezwa haraka na wengine kutupwa gerezani huku Rais Habyarimana akijitetea kwa kisingizio kwamba watu hao ni mapandikizi ya RPF.


Baadae jumuiya ya kimataifa ikiongozwa na ufaransa ilimjia juu Rais Habyarimana kwamba aache kuwachezea akili na badala yake aruhusu demokrasia ya kweli na baraza lake la mawaziri liakisi makundi yote ndani ya nchi ya Rwanda.

Ndipo hapa mwezi April, 1992 ilimbidi Habyarimana kuunda tena upya baraza la Mawaziri na kujumuisha wanasiasa wengine kutoka upinzani japokuwa bado ilikuwa ni kwa uchache sana.

Viongozi hawa wa vyama vya upinzani ndio ambao walifanikisha kufanya mazungumzo na Kagame mwezi July mwaka huo huo 1992 na kukubaliana kusitisha kwa muda mapigano na vikosi vya serikali.


fbfb248aa1ef4778bba472de2afd2b4d.jpg

Arusha International Conference Center



Hapa ndio mwanzo wa mzungumzo ya amani Arusha, hapa Tanzania.


Tanzania tulibebeshwa zigo la kuongoza mazungumzo haya ya amani na jumuiya ya kimataifa kutokana na nchi yetu kuwa chimbuko la mambo mengi hapa Afika Mashariki na ukanda huu wa maziwa makuu. Hii pia ilitokana na turufu ya Tanzania kuwa nchi ya kimkakati kidiplomasia na kuwa ndiyo nchi pekee iliyo karibu na Rwanda ambayo walau tulikuwa tunaonekana tuko 'neutral' kwenye mzozo huo tofauti na nchi kama Uganda, Zaire na Burundi.


Mazungumzo haya ya kurejesha amani nchini Rwanda yaliyokuwa yanaendelea pale Arusha yalikuwa yanahusisha pande nne.


Upande wa Kwanza ulikuwa unaundwa na wahutu wenye msimamo mkali ambao walikuwa wanaongozwa na familia ya mke wa Rais Habyarimana, Bi. Agathe Habyarimana. Hawa waliwakilishwa na chama cha CDR (Coalition for the Defence of the Republic) pamoja na watu wenye msimamo mkali ndani ya chama tawala cha MRND.

Kundi hili japokuwa walikuwepo kwenye mazungumzo haya ya amani Arusha lakini walikuwa wanaupinga mchakato mzima. Walikuwa hawataki kuacha upenyo wowote wa RPF au watusi kumegewa madaraka ya nchi na walikuwa wanawaona watusi wote ndani ya Rwanda ni maadui zao na suluhisho bora zaidi labda wahamishwe wote kutoka Rwanda la sivyo 'watawahamisha' kwa lazima.

Hili lilikuwa ni kundi la kwanza.


Kundi la pili walikuwa ni vyama vya upinzani (ukiindoa CDR japokuwa navyo vilikuwa vinaendeshwa na wahutu). Hawa walikuwa na msimamo wa kati. Walikuwa wako tayari kwa mazungumzo na kumaliza mgogoro huo mezani. Lakini pia walikuwa hawana imani na RPF wakiwaona kama vile ni watu wanaojaribu kuharibu itikadi ya Mapinduzi ya mwaka 1959 ambayo yalianzisha utawala wa Kihutu ndani ya Rwanda.


Kundi la tatu lilikuwa ni RPF. Hapa naomba watu tufahamu kitu kimoja muhimu sana. Kagame alihudhuria mazungumzo haya ya amani kinyume kabisa na matakwa ya wenzake, washauri wake wakuu na makamanda wa ngazi za juu wa RPF. Washauri wake na makamanda wenzake na viongozi wote wa RPF walikuwa kinyume kabisa na mazungumzo hayo ya Arusha na walikuwa na sababu ya msingi kabisa. Hawakuona kundi lolote kwenye hayo mazungumzo ambalo walikuwa tayari kukubali watusi kujumuishwa kwenye uongozi wa nchi na kuishi kama raia halali ndani ya Rwanda. Kwa hiyo hawakuona sababu ya wao kushiriki mazungumzo hayo na waliyaona kama ni njia ya kuwarudisha nyuma kwenye harakati yao ya kuichukua Rwanda kijeshi.

Lakini Kagame aliona kiti cha tofauti kabisa… alikuwa anajua fika kabisa kwamba wenzake kwenye mazungumzo yale hakuna upande wowote ambao ulikuwa na nia njema na RPF na watusi. Lakini Kagame ikumbukwe kwamba alikuwa amefanikiwa sana kujenga taswira chanya ya RPF ulimwenguni (kumbuka ambavyo nilieleza nidhamu ambayo aliwawekea wanajeshi wake). Hakutaka kabisa kupoteza karata hii muhimu ya taswira chanya ya RPF kwenye jumuiya ya kimataifa. Kwa hiyo alishiriki mazungumzo hayo ili kuonyesha jumuiya ya kimataifa kwamba yeye na RPF yake wanataka suluhu ndani ya Rwanda na nia yao ni njema na safi kabisa, japokuwa uhalisia wa moyoni mwake na lengo lake kuu lilikuwa ni kuiweka Rwanda mikononi mwake.

Hili lilikuwa ni kundi la tatu.


Kundi la nne lilikuwa ni wa wawakilisbi wa Rais Habyarimana mwenyewe. Huyu yeye alitawaliwa na woga wa kupoteza madaraka. Kwa hiyo hadharani aliongea kama mtu ambaye yuko tayari kufanya suluhu na kushirikisha makundi mengine kwenye uongozi wa nchi lakini nyuma ya pazia alikuwa anafanya kila awezalo kukwamisha mazungumzo hayo.


7439d7b8176a7d306faa4558c9d899ab.jpg



Mazungumzo Arusha yalichanja mbuga huku kila upande ukiwa na nia yake moyoni.


Katika mzungumzo yale ndipo hasa rangi halisi za Rais Habyarimana zilionekana. Habyarimana alijidhihirisha kabisa kwamba lengo yake kuu lilikuwa ni madaraka haijalishi ni nini anatakiwa kufanya. Kama ni kuua watusi ili abaki madarakani basi ataua. Kama ni kusaliti wahutu wenzake ili abaki madarakani basi atafanya. Mazungumzo ya Arusha yalidhihirisha wazi kabisa kwamba Habyarimana hakuwa na nia yoyote moyoni 'kutetea' wahutu wenzake bali kitu pakee ambacho kilikuwa muhimi kwake ni madaraka.


Kutokana na mzungumzo kwenda kwenye muelekeo ambao ulikuwa unatoa picha kwamba suluhu inaweza kupatikana, wahutu wenye msimamo mkali wakiwakilishwa na chama cha CDR walijitoa kwenye mzungumzo hayo. Lakini hii haikuzuia mazungumzo kuendelea.


Mwezi August 1992 pande zote zilizopo pale Arusha walifikia makubaliano ya kuridhisha kabisa. Walikubaliana kwamba inapaswa iundwe serikali ya umoja wa kitaifa ambayo itajumuisha pande zote ndani ya Rwanda yaani chama tawala MRND, wapinzani na RPF.


CDR na wahutu wenye msimamo mkali ndani ya MRND walikataa vikali makubaliano hayo japokuwa tayari walikuwa wamejitoa kwenye mchakato wa majadiliano. Kuonyesha hasira zao wakaanza tena chokochoko za kuua watusi ili kuwakatisha tamaa RPF kwenye mzungumzo.

Katika usiku mmoja eneo la linaloitwa Kibuye, nyumba mia tano za watusi zilichomwa moto na watu 85 kuuwawa kwa kukatwa mapanga.


Kagame na RPF wakafumbia macho chokochoko hizi na kuendelea kuwepo kwenye majadiliano Arusha.


Mwanzoni mwa mwaka 1993 majadiliano yalifikia hatua nzuri zaidi na pande zote kutia saini mkataba maalumu wa makubaliano. Walikubaliana kwamba iwepo serikali ya umoja wa kitaifa ambayo itajumuisha pande zote isipokuwa chama cha CDR na wahutu wenye msimamo mkali. Serikali hii itakuwa ya mpito na kusimamia mchakato wa kuhakikisha kuwa kunafanyika uchaguzi huru na wa haki na ili kupata serikali ya kudumu.


CDR na wahutu wenye msimamo mkali pamoja na 'zero metwork' (akazu) waliona hili kama ni tusi kubwa sana kwao. Kwanza walijiona wao kuwa ndio wenye haki ya kutawala Rwanda alafu wameachwa nje ya mpango huo wa kuunda serikali ya Kitaifa. Pili waliona ni tusi kubwa kwao na dhidi ya Mapinduzi ya mwaka 1959 kuwajumuisha Watusi kwenye uongozi wa nchi.


Ilifikia hatua mpaka katibu mkuu wa chama tawala cha MRND Bw. Mathieu Ngirumpatse alitoa tamko kudai kwamba chama chake hakitambui makubaliano hayo na wala hawawezi kuyaheshimu. Tamko hili lilikuwa kinyume kabisa na Rais Habyarimana na wawakilishi wa MRND kwenye mazungumzo kule Arusha.


Ndipo hapa walifikia uamuzi kwamba adui yao wa kwanza ni Rais Juvenile Habyarimana. Wanapaswa kumshughulikia yeye kabla ya kuwashughulikia 'adui' yao mkuu wa siku zote, Watusi.


Rais Habyarimana pia alijua hila hizi ambazo zilikuwa zinapangwa na Wahutu wenzake dhidi yake. Akamua kuchukua hatua ya kufifisha ushawishi wa Akazu kwenye serikali yake. Akaanza kuwaondoa kwenye nafasi zote nyeti ambazo aliwaweka awali. Zoezi hili halikuwa si rahisi kwani alipata upinzani mkubwa kutoka kwa Wahutu wenzake hadi kufikia hatua ya kutishiwa kufanyiwa mapinduzi ya kijeshi. Kwa hiyo licha ya kuondoa akazu kwenye sekta na idara muhimu ilimlazimu kuwaacha baadhi.


Kati ya akazu ambao aliwaacha na alikuja kujutia baadae walikuwa ni Augistin Ndindiliyimana ambaye alikuwa ni Mkuu wa Jeshi la Polisi pamoja na Théoneste Bagosora ambaye alikuwa mnadhimu mkuu wa jeshi.


Kutokana na makubaliano ambayo Habyarimana aliyafanya na RPF na mkakati wake wa kuwaondoa akazu kwenye nafasi muhimu, ndipo hapa ambapo wahutu wenye msimamo mkali kwenye kila idara na taasisi waliyopo walianza kutengeneza 'idara' mahususi za pembeni zenye kujumuisha wahutu wenye msimamo mkali. Yaani kila idara au taasisi walikuwa wanaunda idara pacha pembeni yake ambayo wanachama wake ni wahutu wenye msimamo mkali tu. Yaani tuseme kwa mfano Idara ya Usalama wa Taifa, akazu wanaunda 'idara' ndogo ya pembeni ya wahutu wenye msimamo mkali pekee.


Na ni hapa na katika kipindi hiki ndipo ambapo wazo la 'mauaji ya kimbari' lilizaliwa. Kwamba wanapaswa kufanya kile ambacho jina lao linaakisi, 'Zero Network'.

Wanapaswa 'kuisafisha' Rwanda. Wanapaswa kuhakikisha hakuna mtusi anayetembea juu ya ardhi ya Rwanda. Wanapswa kufanya 'suluhisho' la kudumu juu ya tatizo lao hili la Watusi.




Sehemu ya 10 itaendelea leo jioni…



SEHEMU YA 10


cadf94c44b1e7f4568775524196473fb.jpg


Le Clan de Madame



Mkataba wa makubaliano ambao ulisainiwa Arusha kwa kiasi kikubwa ulikuwa chanya kwa pande zote na kila mtu, yaani Kagame, Habyarimana na vyama vya upinzani waliridhia kabisa mkataba huo.


Lakini shida ilikuwa kwa Wahutu wenye msimamo mkali chini ya CDR na hata ndani ya MRND. Wengi wao hawakukubali mkataba huo kwa sababu moja kuu, kuona kwamba ati watusi warejee kuwa sehemu ya uongozi wa nchi.

Kwao hili waliona na tusi zito na kitu ambacho abadani hawawezi kukikubali.


Vuguvugu hili likapamba moto na wahutu wenye msimamo mkali wakiongozwa na kikundi kidogo cha watu wenye ushawishi mkubwa serikalini ambao walijiita 'le clan de madame' (inner circle ya akazu).


Walianza kuratibu maandamano ya Wahutu nchi nzima kupinga mkataba ambao Rais Habyariamana alitiliana saini na RPF.

Kwa kuwa japokuwa walikuwa wanafanya maandamano lakini bado serikali ya Habyarimana haikuwasikiliza wala kurudi nyuma kwenye mkataba wake na RPF, hivyo wakaamua kwenda mbali zaidi. Wakaanza tena mauaji dhidi ya Watusi.


Mauaji haya yalifanyika zaidi maeneo ya Kaslazini Magharibi mwa Rwanda na yalidumu kwa muda wa siku sita mfululizo wakishuhudia mamia ya watusi wakiuwawa na nyumba zao kuchomwa moto na Wahutu. Mara ya kwanza Kagame hakutaka kufanya chochote kile au kuchukua hatua za kijeshi zozote akiamini kwamba umebaki muda mchache watakuwa sehemu ya serikali na watahakikisha kwamba mauaji hayo yanakoma.


Ubaya ni kwamba kama nilivyoeleza kuwa Rais Habyarimana alikuwa anaheshimika na Wahutu wenye nguvu kutokana na mkewe kutoka kwenye familia yenye ushawishi mkubwa nchini humo. Kwa lugha nyingine tunaweza kusema kwamba Rais Habyarimana alikuwa kama amewekwa kiganjani kimaamuzi na alikuwa hawezi kufanya lolote bila mkewe kukubali. Hii ndio sababu ambayo ilimfanya ashindwe kufanya lolote pale ambapo akazu walianza kuratibu mauaji dhidi ya Watusi. Na mkewe abadani asingeliweza kukubali watu wake wa 'le clan de madame' kuchukuliwa hatua.


Kwa hiyo mauaji dhidi ya Watusi yaliendelea sehemu mbali mbali na serikali ya Habyarimana ilishindwa kufanya chochote licha ya kusaini makubaliano ya amani na RPF.


Nimeeleza kwamba mwanzoni Kagame hakutaka kuchukua hatua yoyote ya kijeshi dhidi ya mauaji yaliyokuwa yanaendelea ili kuheshimu mkataba ambao walisaini Arusha.

Lakini kuna jambo moja lilitokea.


Watusi ambao miji yao ilivamiwa na kuanza kuuwawa, baadhi yao walifanikiwa kutoroka kutoa kwenye miji hiyo na kukimbilia kwenye maeneo ambayo yalikiwa yanashikiliwa na RPF ili kuokoa maisha yao.

Watu hawa ambao walikimbilia kwenye maeneo yaliyo chini ya RPF kuna siku walikutanishwa na Kagame na kuongea nao. Walimsimulia kinaga ubaga namna ambavyo Watusi wananyanyasika na kuuwawa kama wanyama wa mwituni hapo Rwanda. Inaelezwa kwamba siku hii ilikuwa ni moja kati ya siku chache sana ambapo Kagame alishuhudiwa machozi yanamtoka hadharani kutokana na simulizi hizo za mateso ya Watusi ambazo alisimuliwa na watu hao waliotoroka kutoka mikononi mwa Wahutu.


Ndipo hapa pasipo jumuiya ya kimataifa kutegemea, Kagame akatoa tamko rasmi kwamba yeye na RPF wanajitoa kwenye mazungumzo ya amani ya Arusha na pia wanajitoa kwenye mkataba wa amani uliosainiwa.

Alijenga hoja kwamba haoni dhamira yoyote ile ya serikali kuzuia mauaji dhidi ya watusi ambayo yalikuwa yanaendelea nchini Rwanda hivyo wanachukua jukumu mikononi mwao kukomesha mauaji hayo yanayoendelea.


Ilikuwa tayari imepita miezi sita tangu mapigano ya RPF na vikosi vya serikali yasimame ili kupisha mazungumzo ya amani Arusha. Na leo hii baada ya miezi sita Rwanda ilikuwa inarejea tena vitani.


Siku hii ilikiwa ni February 8, 1993.


c79fe35671df0f123961618caaaf7192.jpg


Hivyo basi siku hii ya February 8, 1993 RPF wakarudi tena vitani dhidi ya majeshi ya serikali.

Mapigano ya safari hii RPF hawakupata upinzani mkubwa kama miezi sita nyuma. Walikuwa wanawashinda vikosi vya serikali kwa urahisi sana na kuyaweka maeneo mengi zaidi kwenye himaya yao.


Shida kubwa ambayo walikuwa nayo vikosi vya serikali ni morali ndogo, nidhamu na uzoefu.

Katika kipindi hiki uchumi wa Rwanda ulikuwa umetetereka kwa kiasi kikubwa sana kutokana na serikali kutumia fedha nyingi kugharamia vita kwa miaka kadhaa. Sarafu ya Rwanda pia, faranga, ilikuwa imeshuka thamani kwa kiwango cha kutisha dhidi ya dola ya marekani.

Hivyo serikali ya Rwanda ilikuwa haina fedha ya kutosha kulipa wanajeshi wake mishahara kwa wakati. Na hii ilishusha mno morali ya wanajeshi.

Lakini pia katika kipindi hiki serikali kutokana na woga na kujihami walikuwa wameongeza ukubwa wa jeshi kutoka wanajeshi 10,000 mpaka kufikia wanajeshi 30,000 ndani ya muda mfupi sana. Wanajeshi hawa hawakuwa na uzoefu wa uwanja wa vita na pia hawakuwa na nidhamu ya kiaskari. Mara nyingi waliripotiwa kuvamia raia na kubaka wanawake na kuua wengine.


Hivyo basi licha ya Kagame kuwa na wanajeshi wachache mno kulinganisha na vikosi vya serikali, lakini waliwazidi weledi wa kijeshi, nidhamu na uzoefu. Na hii ndio sababu ya RPF safari hii kuwapiga vikosi vya serikali kwa urahisi mno.


Vikosi vya RPF vilipigana kutokea Kaskazini mwa Rwanda na kushuka kusini. Waliiweka tena Ruhengeri kwenye himaya yao ndani ya siku moja tu ya mapambano. Kesho yake wakaichukua Byumba na kuendelea kuchukua mji baada ya mji.


Rwanda ilishuhudia kwa mara nyingine tena maelfu kwa maelfu ya wahutu wakikimbia miji yao kwenda kwenye maeneo yaliyo chini ya vikosi vya serikali ili kuwakimbia RPF.


Mtikisiko huu mkubwa wa ushindi wa RPF kila siku ulifika mpaka Ufaransa ambao walikuwa wanamfadhili kwa kiasi kikubwa Rais Habyarimana kutokana na wao kuwa na maslahi ya moja kwa moja ndani ya Rwanda.

Kwa kupaniki, serikali ya ufaransa ikatuma vikosi vya wanajeshi wake kuja Rwanda kusaidia vikosi vya serikali kuwadhibiti RPF.


Baada ya vikosi vya wanajeshi wa Ufaransa kuwasili angalau waliweza kuwatikisa RPF kwa siku kadhaa na kutoa upinzani halisi wa kijeshi. Lakini hii ilikuwa ni kwa siku chache mno kabla ya RPF kurudi tena kwenye ubora wake na kuwadhibiti sawasawa vikosi vya serikali na Ufaransa kwa pamoja.


Mpaka kufikia February 20, 1993… RPF walikuwa wamebakiza kilomita 30 tu kuingia mji mkuu wa Kigali. Wachambuzi karibu wote wa masuala ya medani za vita wanakubaliana kwamba kama RPF wangefanya shambulizi mara moja tu kwa nguvu ambayo walikuwa nayo na kwa jinsi walivyokuwa wamewadhibiti vikosi vya serikali na Ufaransa basi wangeweza kuiweka Kigali mikononi mwao na kujitangazia ushindi.


Lakini Kagame alifanya kitu cha ajanu ambacho mpaka leo hii yawezekana ni yeye mwenyewe pekee akilini mwake ndiye anaelewa kwa nini alichukua maamuzi yale.


Kagame hakuishambulia kigali wala kuingiza wanajeshi wake. Na hakuishia hapo tu, akatangaza kusitisha mapigano dhidi ya vikosi bya serikali.!!


Hii ilikuwa ni ajabu kweli kweli. Hakuna ambaye alitegemea au kutarajia kitu hiki. RPF walikuwa wameshinda nguvu vikosi vya serikali na shambulizi dogo tu lilitosha kuiweka Kigali kwenye himaya yao. Kwa nini Kagame hakutaka kuishambulia Rwanda? Na kwa nini aliamua kutangaza kusitisha mapigano?

Hakuna anayejua zaidi ya Kagame mwenyewe…


Suala hili liliwachkukiza mno makamanda wenzake wa ngazi za juu wa RPF na kukatokea sintofahamu kubwa sana nusura kuipasua RPF.


f03a55674f0e35b8d96960eee4a2e4df.jpg


Lakini suala moja hatupaswi kusahau ni kwamba, Paul Kagame ni "master of psychological warfares".

Ni mtu mwenye kujua mno na ustadi wa hali ya juu kupambana kisaikolojia na kucheza na akili ya adui.



Binafsi, moja ya masuala ambayo yamenifikirisha sana wakati wa kuandaa makala hii basi ni hili tukio, kwa nini Kagame aliamua kutoshambulia Kigali siku ile ya February 20? Kwa nini aliamua kutangaza kusitisha mapigano?


Nikajaribu kuvaa viatu vyake na kuona kile ambacho Kagame alikuwa anakiona… (unaweza pia kunipa maoni yako inbox).


Katika tafiti zangu kuhusu makala hii jambo moja ambalo nimeliona ni ongezeko la silaha za kisasa kwa RPF katika kipindi hiki (February 1993). Silaha hizi zilikuwa zinachukuliwa kutoka kwa wanajeshi wa serikali kila mahala ambapo wanakuwa wamewashinda.

Hapa naona vitu viwili… Kagame alikuwa anataka kulimega jeshi la serikali vipande vipande bila kuwabakisha na kiwango kikubwa cha silaha kabla hajaichukua Rwanda. Kama angeliichukua Rwanda haraka hivi na Wahutu wenye silaha kukimbilia msituni wakiwa na kiwango kikubwa hivi cha silaha yawezekana mpaka leo hii bado Rwanda kungelikuwa na vita.


Sababu ya pili naamini Kagame alikuwa anajaribu kuwavuta zaidi jamii ya kimataifa kuwa upande wake na hakutaka kuonekana ni mroho wa madaraka.

Kwamba alikuwa anajaribu kuonyesha jamii ya kimataifa kuwa ana uwezo wa kuiweka Rwanda kiganjani mwake muda huo, lakini hakufanya hivyo ili kuwaonyesha kuwa haitaji madaraka (japo hilo ndilo lengo lake kuu) bali anataka amani Rwanda.


Huko nyuma Kagame alishafanikiwa kutengeneza taswira chanya kwa jamii ya kimataifa juu ya vikosi vyake vya RPF na kutokana na tukio hili Kagame alifanikiwa mno kupata mioyo ya viongozi wengi wa Kimataifa kuwa upande wake.

Na pia kama angeliichukua Rwanda kwa ushindi wa mara moja na kuindoa serikali iliyoko madarakani na kuingiza serikali yake… ingeweza kutafsiriwa kama amepindua wahutu na kuwarejesha watusi wenzake kwenye utawala wa Rwanda na ingeweza kuchochea vita isiyo na kikomo ya wenyewe kwa wenyewe kati ya wahutu na watusi. Na hili ndilo sababu hasa mpaka wamefikia hatua hii ya nchi kuwa vitani muda wote huo.


Pia au labda alikuwa anasubiri sababu kubwa zaidi ya kuhalalisha yeye kuchukua madaraka ya kuingoza Rwanda. Sababu kubwa zaidi ambayo hata jumuiya ya kimataifa itamuunga mkono na wasimuangalie kama mpenda madaraka.


Tukumbuke kwamba kagame ni 'born tactician, every move he makes means something.!'


Sababu hasa ya kufanya maamuzi ambayo aliyafanya February 20, 1993 ni yeye mwenyewe anaielewa.


Suala hili lilizua mpasuko mkubwa sana ndani ya RPF. Makamanda wenzake wakinung'unika kuwa amewanyima ushindi. Wengine bado wakilazimisha kwamba waivamie Kigali.

Lakini Kagame kutokana na nguvu aliyokuwa nayo na ushawishi wake akafanikiwa kuzima kelele zote hizi za wenzake na kufuata kile ambacho alikuwa amekiamua.


Ujumbe mkubwa zaidi ambao RPF walikuwa wameutuma kwa dunia ni kwamba RPF walikuwa na nguvu na weledi wa vita kuwazidi vikosi vya serikali.


Na Habyarimana alilijua hili. Hakutaka kuchelewa kabla 'mchele' haujamwagika wote. Safari hii ni yeye akamuomba Kagame warudi tena kwenye meza ya majadiliano.


Kagame alikubali. Siku mbili baadae walirejea kwenye meza ya majadiliano. Lakini safari hii kwa kuwa ni Habyarimana ndiye ambaye aliomba kurejea kwenye meza ya majadiliano hii ilimpa mwanya Kagame kutoa masharti yale ambayo alikuwa anayataka.


Mazungumzo haya hayakuwa Arusha tena kama awali, bali safari hii yalifanyika 'nyumbani' Uganda msuluhishi akiwa Rais Yoweri Museveni na wawakilishi kadhaa wa nchi za Ulaya. Hii ndio inaitwa kesi ya nyani kumpelekea ngedere.


Kagame alikuwa anawachezesha ngoma ambayo walikuwa bado hawajaijua… na muda si mrefu alikuwa anafikia lengo lake.





Itaendelea…




SEHEMU YA 11



Kwenye sehemu ya kumi tulijadili namna ambavyo serikali ya rais Habyarimana walifikia makubaliano na RPF ya kusitisha mapigano lakini baadae mauaji ya watusi yaliendelea na kumfanya Kagame kuanza tena mashambulizi na kulishinda jeshi la serikalinkwa urahisi kabisa.

Tuliona namna ambavyo Habyarimana safari hii aliomba mazungumzo na Kagame ili kusitisha makubaliano.



Tuendelee…



Mazungumzo ya Uganda yalichukua siku mbili na kisha kurejea tena Arusha.

Nchi za Ulaya zilikuwa zinamtaka Kagame arejeshe nyuma vikosi vyake kurudi kwenye eneo ambalo walikuwa wanalishikilia kabla ya February.


Baada ya mabishano makali ya siku kadhaa huku Kagame akitishia kwamba ataanza tena mashambulizi dhidi ya vikosi vya serikali.


Ndipo hapa ambapo pande zote mbili walifikia makuabaliano.


Kwamba;


Kagame atarudisha nyuma vikosi vyake mpaka kwenye maeneo ambayo walikuwa wanayashikilia kabla ya mwezi February, 1993. Lakini maeneo hayo mapya ambayo RPF walikuwa wameyaweka kwenye himaya yao baada ya Febrary, pindi tu RPF wakirejesha nyuma vikosi vyao kutokana na makubaliano hayo basi maeneo hayo yatatengwa kama 'De-militarised zone'. Kwamba serikali haitaruhusiwa kuingiza wanajeshi wake kamwe kwenye maeneo hayo.


ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog