Search This Blog

Thursday 29 December 2022

KIGUU NA NJIA - 5

 

  Simulizi : Kiguu Na Njia

Sehemu Ya Tano (5)


Niliichekelea sana fursa hiyo. Kwanza ingenipa fursa ya kupumua hewa safi ya nje. Hewa asilia ya oksijeni itokayo katika mimea na kusambazwa na upepo badala ya hii tuliyokuwa tukiitumia ambayo sikujua ilitokea wapi. Lakini pia kufikia Zanzibar ilikuwa ndoto yangu ya muda mrefu. Toka nchi hizi zilipoungana na sifa za Karume za mapenzi kwa nchi yake zikiimbwa katika vyombo vya habari azma yangu ya




kukanyaga ardhi ya nchi hiyo ilikuwa ikiongezeka siku baada ya siku.

Toka wakati ule ningali belubelu bado, mkakati wangu wa kufanya biashara ya chumvi kati ya Zanzibar na Bagamoyo ulipokwama, niliishia kujifariji kwa kusoma na kusikiliza tu, kila kilichozungumza juu ya nchi hiyo. Nilijifunza kuwa ilikuwa moja ya nchi zenye historia pekee duniani. Kwa mfano, wataalamu wa historia wanaamini kuwa miji katika visiwa hivyo ni vya kale kuliko nchi nyingi za dunia. Inaaminika kuwa waanzilishi wa taifa hilo makabila ya Wahadimu na Watumbatu walianza kuishi katika visiwa hivyo, wakitokea katika pwani za Afrika Mashariki miaka 1000 iliyopita. Watu hao waliishi katika vijiji vidogovidogo vya ukoo, bila uongozi wa pamoja jambo lililofanya wakose uwezo wa kutetea haki yao ya umiliki pale walipoanza kuingia katika visiwa hivyo.

Wafanyabiashara toka nchi za Kiarabu hasa Iran na Iraq na Wahindi wanaelezewa kufanya biashara na nchi hiyo miaka nenda rudi. Katika karne ya 11 na 12 baadhi ya wafanyabiashara hao walianza kuifanya Zanzibar makazi yao ya kudumu wengi wao ikiwa pamoja na kuanza kuoana na wenyeji. Matokeo ya ndoa ni kuibuka kwa watawala kama Mwinyi Mkuu au Jumbe miongoni mwa wahadimu au mashaha miongoni mwa Watumbatu. Viongozi hao hawakuwa na nguvu nyingi. Lakini angalau walisaidia kulinda uhalisia katika makabila yao.

Yule naodha machachari wa Kireno, Vasco da Gama, alifika Zanzibar ,waka 1499 na kufungua njia ya wageni wa kutoka Ulaya nchini humo. Mwaka 1505 nchi hiyo ilifanywa koloni la Ureno pale walipoamua kuiteka kabisa.

Mwaka 1698 Zanzibar ikafanywa sehemu ya mali

za Oman, hatua iliyofuatiwa na Sayyid Said bin Sultan al




Busaid ambaye akiwa na umri wa miaka 15, mwaka wa 1806 kuhamishiwa makao yake ya kifalme mjini humo. Baadaye utawala wa pamoja wa Zanzibar na Oman uligawanyika mwaka 1861 baada ya kifo chake, wanawe ambao walikuwa wakigombea madaraka walipofikia uamuzi wa Sayyid Majid bin Said alipochukua madaraka ya na Zanzibar na ndugu yake Sayyid Thuwaini kuwa Sultan wa Oman.

Baada ya hapo historia ya Zanzibar ina mlolongo mrefu wa kugombea au kupokonyana madaraka baina ya Waarabu na Waarabu, Wajerumani kwa Waingereza na hatimaye Waarabu kwa Waingereza. Ni pilikapilika za aina hiyo zilizofanya Zanzibar iingie katika historia kama nchi iliyovunja rekodi kwa kupigana vita fupi kuliko zote duniani. Vita hiyo ilipiganwa kwa dakika 45 tu. Ilikuwa baina ya majeshi ya Uingereza na yale ya Sultan Sayyid Khalid bin Bargash ambaye, alipokonya madaraka na kujitangaza Sultan wa nchi hiyo wakati Waingereza waliamini mtawala halali angekuwa Hamoud bin Mohamed. Waingereza walimwamuru Bargash kuachia madaraka; akakataa. Wakampa muda wa kuondoka huku manowari zao zikiwa baharini tayari kupiga mizinga iwapo angeendelea kukaidi. Muda waliompa ulipokwisha manowari hizo zililipua mizinga ambayo ililiharibu jengo la Beit al Hokum. Majeshi ya bargash yalijaribu kujibu kwa bunduki zao lakini hazikufua dafu. Dakika 45 baadaye Bargash alikimbilia katika ubalozi wa Ujerumani, vita ikasimamishwa na Maoud bin Mohamed akatawazwa kuitawala Zanzibar.

Utawala wa Mwingereza nao ulikoma katika kisiwa hicho mwaka 1963 pale nchi hiyo ilipotoa uhuru na uchaguzi ulipofanyika muungano wa ZNP na ZPPP uliposhinda kwa hila dhidi ya ASP ya wazalendo akina Abeid Aman Karume na kufanya Waarabu waendelee kuwa madarakani. Utawala




huo haukudumu. Mwaka mmoja baadaye, Januari 12, 1964 wazalendo walipindua serikali hiyo na uongozi kuwekwa chini ya Karume.

Hayakuwa mapinduzi rahisi kama mtu unayeweza kufikiria Waarabu wengi wanadaiwa kuuawa, maelfu wengine wakitupwa gerezani. Aidha, Karume alitumia mapinduzi hayo kurejesha hadhi ya mtu mweusi kwa kutoa amri mwanamume kuoa mwanamke yeyote wa Kiarabu au Kihindi anayempenda. Amri chungu ambayo ilipigiwa kelele na baadhi ya nchi duniani, lakini kwa nchi iliyobobea kwa ukandamizaji, ambayo wakati fulani iliaminika kuwa robo tatu ya raia wake walikuwa watumwa wa Waarabu hatua ipi zaidi ingeweza kurejesha usawa na umoja haraka zaidi ya zile ndoa za lazima?

Misuguano ya ndani na vitisho toka nje kwa taifa hilo dogo ilikoma pale nchi hiyo ilipoungana na Tanganyika na kuzaliwa taifa jipya la Tanzania april 12, 1964 ikiwa miezi mitatu tu baada ya mapinduzi.

Hiyo ndiyo Zanzibar ya kale, ambayo kudra za Mungu

ziliniwezesha kuwa safarini kuiendea.

Mfungwa hachagui njia, mfungwa hachagui siku ya safari. Yeye ni mtu wa kukurupushwa tu, kama mifugo. Ndivyo ilivyokuwa kwetu. Fununu za safari zilianza ghafla kwa minong’oni baina ya wafungwa. “Skochi jamani…. Skochi ya Zanzibar…’ zilivuma taarifa hizo katika selo. Nadhani ‘skochi’ ni lugha moja ya zile lugha za kijelajela iliyokuwa na maana ya ‘escort’ kwa kiingereza kwani mfungwa haendi popote bila askari jela wa kuwasindikiza.

Sikujua Kama ningekuwa mmoja wa wateule hao hadi siku ya safari, jina langu lilipoitwa na kuamriwa kupanda karandinga. Tulikuwa kama wafungwa mia hivi na askari kumi wa kutulinda. Safari yetu ilianza asubuhi ya jumatatu





moja, tukaifuata barabara ya Dar es Salaam. Tulipofika Moshi tulisimama kwa nusu saa, mkuu wa safari aliposhuka kupata kifungua kinywa.

Nilitamani kuuona mji wa Moshi kwa mara nyingine, lakini niliishia kuuchungulia tu kupitia katika nyavu za waya za karandinga letu, hali ya hewa ilikuwa ileile, tamu inayosisimua. Mlima Kilimanjaro uliendelea kuinamia mji, kama unaolinda kwa maovu, kwa utukufu wake. Kitu kilichonivutia zaidi kwa mji wa Moshi ni usafi. Barabara zilikuwa zikimeremeta, majengo yaking’ara kwa rangi. Ilikuwa nadra sana kuona uchafu ukizagaazagaa mitaani kama ilivyo miji mingi niliyopata kuitembelea.

Safari ilipoanza tena nilikuwa tayari nimepata upenyo mzuri wa kuchungulia nje. Barabara safi, ya lami ilikuwa ikiteleza chini ya matairi ya gari letu kwa uhakika kabisa. Tulikuwa tukielekea Mashariki hadi tulipofika Himo ambapo kuna njia panda ya kuelekea Taveta nchini Kenya na ile ya Dar es Salaam ambayo kwa kiais fulani ilielekea Kusini. Tulipita Kifaru, tukaingia Mwanga. Toka hapo niliweza kuliona kwa mbali bwawa la nyumba ya Mungu. Tukateleza hadi Same, Hedaru, Mkomazi, Mombo na baadaye Korogwe ambapo tulipumzishwa katika gereza moja dogo ambalo sikubahatika kufahamu jina lake. Hapo tulipewa chakula na kutakiwa kumaliza haja zetu za kimaumbile, kubwa na ndogo kabla ya kuanza safari.

Tulifika Segerea na kuiacha barabara inayokwenda Tanga hadi Mombasa tukashuka na kuvuka mto Wami hadi Msata. Hapo viongozi wetu wa safari walisimama kwa muda kujadiliana, ama wafuate barabara ile ndogo isiyo na lami ambayo inachepuka hadi Kiwangwa, Kilola na hatimaye Bagamoyo au ile iliyozoeleka, lakini ya mzunguko, ambayo




ingetufikisha Chalinze, Mlandizi na Kibaha kabla ya kuingia Dar es Salaam. Kumbe safari yetu ya Unguja ilikuwa ianze Bagamoyo. Nadhani kwa usalama wao au wetu waliamua kupita njia ndefu ya Dar es Salaam.

Nilishangazwa na wingi wa watu na majengo niliyoyaona hasa kutokea Mlandizi, mara tu baada ya kuvuka mto Ruvu. Nilipopita kwa mara ya kwanza eneo hili lilikuwa pori la kutisha ambalo lilimilikiwa na nguruwe mwitu na ndege wa porini. Sasa lilijaa binadamu na majengo tele. Wakati huo ilikuwa usiku wa saa tatu hivi, lakini taa za umeme toka maeneo mbalimbali, wingi wa magari barabarani na watu tuliwapitia kando ya barabara uliashiria wingi wa watu na pilikapilika nyingine za kibindamu.

Pilikapilika hizo ziliongezeka maradufu mara tulipoingia Mbezi na hatimaye Kimara. Gari letu lilikwenda kwa mwendo wa kinyonga kutokana na msongamano wa magari. Kandokando mwa barabara, kulia na kushoto, nilishangazwa na wingi wa baa za pombe na wateja waliofurika kelele za muziki wa kileo, ambao baadaye niliambiwa kuwa unaitwa Bongo flavour ziliweza kusikika ndani ya gari hiyo kwa uwazi kabisa. Katika baa moja mwanamuziki mmoja alikuwa akicheza kwa nguvu zake zote;

Kuku kapanda baiskeli, Bata kavaa raizoni…

Wimbo huo ulitufikia vizuri kabisa katika gari. Wengi wetu ambao tulizowea nyimbo za akina Marijani Shabani, Wema Abdallah au Mbaraka Mwishehe tuliishia kucheka kwa mapinduzi haya ya kisanaa. Hatukujua kama tunakwenda mbele au tunarudi nyuma katika fani hiyo ya muziki.

Zaidi ya nyimbo kitu kingine kilichotufikia ndani ya

gari hilo ni harufu ya nyama choma. Yale mapande ya nyama,




mishikaki na kuku waliokuwa wakiokwa katika mabaa hayo yalisambaza harufu tamu ambayo ilitutia uroho wa nyama, mboga iliyopatikana kwa nadra sana gerezani.

Tulifika Dar es Salaam yapata saa nne na robo usiku. Ule muujiza nilioutegemea ulijidhihirisha. Dar es Salaam haukuwa mji tena bali jiji. Majumba mengi yaliyopanda juu, watu wakiwa tele mitaani muda wote. Biashara ya baa ilishamiri karibu kila mahala. Nchi hii haina biashara nyingine?

Tulitoka Ubungo na kuelekezwa Mwenge. Gari likageuzwa na kuelekea Kaskazini tulikotokea tukifuata barabara ya Bagamoyo. Kwangu barabara hiyo ilikuwa muujiza mwingine. Tofauti kabisa na ile tuliyoitumia na akina Leakey miaka kadha wa kadha iliyopita hii ilikuwa barabara pana ya lami. Na ilifurika magari muda wote. Lile pori la wakati ule halikuwepo tena. Badala yake mji ulikuwa umemeza kila kitu kiasi cha kufanya kambi ya jeshi la Lugalo, ambayo zamani ilionekana kujengwa porini sasa iwe katikati ya mji wa kiraia, ambao ulisambaa hadi Pwani yake uwe hadi ufukwe wa Kunduchi. Vile vilivyojulikana kama vijiji vya Tegeta, na Bunju sasa ilikuwa sehemu ya jiji la Dar es Salaam ambalo lilibakiza kilometa mbili tu kuungana na mji wa Bagamoyo, Bagamoyo ambako tulifikishwa katika gereza la Kigongoni kusubiri safari ya Zanzibar.

Ulipata kusikia kuwa binadamu ana mkia? Kama ulipata, je ulipata kuona mkia huo? Ni watu wachache sana duniani waliopata kuuona; mimi nikiwa mmoja wao. Bahati au balaa hiyo nilikutana nayo katika gereza hilo ambalo ni maalum kwa kilimo.

Awali sikuyaamini macho yangu pale nilipowaona watu wa ajabu. Miili yao ilikuwa inatisha, ngozi ikiogofya. Fikiria ngozi ya mtu yeyote, uliyopata kuiona maishani mwako, fikiria





hata mgonjwa wa UKIMWI aliye taabani sana; bado kamwe hutaweza kumfananisha na miili ya baadhi ya wafungwa tuliokutana nao katika gereza hilo. Walinyauka, walisinyaa na kuifanya miili yao ifikie kiwango hicho cha kutisha. Lakini zaidi ya ngozi ya miili hiyo hali ya kukonda ilitisha zaidi. Baadhi yao, waliokuwa taabani zaidi walionekana kama mifupa iliyounganishwa na aina fulani ya ngozi! Ni pale walipovua mashati ndipo nilipoweza kuona mkia wa binadamu!


Mimi pia nilikuwa mfungwa. Lakini hali ya baadhi ya wafungwa hawa ilinifanya nitokwe na machozi! Nilipouliza nini kinatokea wenyeji walininjibu kwa urahisi tu; Luba.


Luba ndio nini?


Ugonjwa. Unatokana na wadudu ambao hushambulia mpunga. Unajua kilimo cha mpunga kilivyo? Inabidi kuingia katika maji au tope. Kwa mfungwa kulazimishwa kuingia katika maji ya tope linalofika hadi shingoni ni jambo la kawaida. Humo ndimo hukutana na wadudu hawa ambao hushambulia mpunga na hivyo wao pia kushambuliwa.


Msemaji alikuwa mfungwa mzoefu. Ilikuwa vigumu kuamini kweli ni mfungwa kwa jinsi alivyokuwa msafi, kiribatumbo kimejitokeza wazi chini ya kifua chake.


“Ni wajinga,” aliongeza. “Wanaingia kichwakichwa katika miji ya watu. Wangeuliza maradhi hayo yasingewapata.”


“Kwa vipi?” Nilimuuliza.


Alikohoa, kabla hajajibu akisema, “Iko namna. Kuna dawa. Wenzao kabla ya kuzama katika tope lile tunajipaka tumbaku. Wadudu hawatusogelei wala kutudhuru.”


“Kwa nini hamkuwaambia hayo mapema?” nilimsaili. “Si nimekwambia wanaingiamiji ya watu kichwakichwa?”


lilikuwa jibu lake.


Kwa mara ya kwanza nilijisikia kumpiga mtu makonde.








Mtu mwenyewe hakuwa mwingine zaidi ya mzee huyu anayezungumzia maisha ya binadamu wenzake kana kwamba anajadili suala la paka. Ili kuepuka kufanya hivyo nilimwacha akiendelea kubwabwaja na kujiunga na wenzangu tuliokuwa nao katika ‘skochi’.


Nilishukuru pale siku mbili baadaye tulipochukuliwa na magari kuelekea pwani ya Bagamoyo, ambako majahazi mawili yalitupeleka Unguja yalitia nanga yakitusubiri.


Kutoka pwani hiyo hadi Zanzibar ilikuwa safari ya kilometa zipatazo 25 tu, lakini kwa wenzangu wengi ilikuwa safari ndefu, ngumu iliyojaa mashaka. Mawimbi na upepo vilifanya wengi wapatwe na ule ugonjwa uitwao ‘homa ya bahari.’ Baadhi walitapika, baadhi wakiwa taabani kana kwamba wanakaribia kukata roho. Askari wawili waliotusindikiza pia walikuwa wakitapika huku wenzao wakiwacheka.


Wakati tunakaribia kutua pwani tulipata burudani tosha toka kwa pomboo, wale viumbe wa baharini ambao mimi huwaita samaki lakini wataalamu uwachukulia kuwa ni wanyama wa majini kwa kuwa wananyonyesha watoto wao kinyume na samaki wengi, kawaida. Viumbe hawa ambao wengi huwaita ‘Dolphins’ walilizingira jahazi letu, mara kwa mara wakichupa angani na kutuchungulia kwa namna ya kusisimua.


Pomboo, ambao nyama yake ni tamu sana ni viumbe wanaofugika na kufundishwa. Nchi kadhaa tayari wamewafundisha michezo mbalimbali kama kushindana, kuruka kwa pamoja kudaka mpira na mambo mengine tele ambayo huvuta watalii. Baadhi ya nchi zilizoendedelea tayari wanawafundisha kubaini mabomu ya kutegwa baharini na hivyo kuepusha madhara.








Kwangu walikuwa burudani tosha na walitusindikiza hadi tulipotia nanga ufukwe wa Zanzibar, mji mkuu wa nchi hii ambayo inadaiwa iko chini kidogo ya usawa wa bahari. Baadhi ya wataalamu wanadai kuwa iko siku nchi hiyo itamezwa na maji na kutoweka katika uso wa dunia. Lakini hiyo ni hadithi nyingine. Yetu ni kwamba mara tulipofika magari ya wafungwa yalikuwa yakitusubiri tayari kutupeleka katika gereza la kiinua mguu ambako tungepumzika kidogo kabla ya kusafirishwa tena hadi Pemba yaliko mashamba mengi zaidi ya karafuu.


Tulilundikwa katika makarandinga, ambapo hayakutofautiana sana na yale ya bara. Yakatiwa moto na kuondoka. Kwa kiu yangu ya kuufahamu mji wa Zanzibar nilifanya kila jitihada kuhakikisha nachungulia nje na kujionea chochote ambacho ningeweza kukiona. Kwa mbali, niliweza kuiona hoteli maarufu ya bwawani ambayo ilijengwa na serikali ya Karume. Wakati tukipita mitaani, eneo la Kichenzani nilishangaa kuona mitaa yote ikiwa imemezwa na majumba marefu sana, takribani mita mia tano kila nyumba. Nyumba hizi ambazo zilikwenda juu kwa gorofa tatu au nne tu zilielekezwa kuwa ilikuwa kazi nyingine ya Karume kwa wananchi wake alipotoa amri akisema, ‘Wazungu wanashindana kujenga nyumba ndefu kwenda juu kwa ajili ya uhaba wa ardhi yao, sisI tutajenga nyumba ndefu kwa upana.’ Matokeo ya kauli hiyo ndiyo nyumba hIzo ambazo zilikuwa mkombozi kwa wananchi ambao wengi wao walikuwa masikini sana baada ya kukandamizwa na wageni miaka nenda rudi.


Katika eneo la darajani nilishangazwa na wingi wa waendesha baiskeli. Katika maneno fulani ilibidi waongozwe na askari wa barabarani kama ilivyo kwa magari. Eneo hilo lina soko kuu, wenyewe wakiliita ‘markiti’ bila shaka jina








hilo lilitokana na neno ‘market’ la Kiingereza. Kilichonivutia zaidi hapo ni mavazi, kanzu nyeupe ndala miguuni na baragashia kichwani vilitawala mavazi ya mwanaume. Kwa wanawake mabaibui yaliyofunika sura gubigubi yalitamalaki na kunikumbusha miji ya Tanga. Utamaduni mwingine niliobahatika kuuona hapa katika muda mfupi ni kitendo cha wanaume wengi zaidi kuwa na makapu kununua mahitaji ya nyumbani. Ilikuwa nadra sana kuwaona wanawake wakifanya manunuzi hayo.


Tuliiacha darajani na kuambaa pembeni mwa mji mkongwe. Macho yangu yalivutiwa na nyumba za kale, ambazo baadhi zilijengwa zaidi ya miaka mia mbili iliyopita lakini bado zinatumiwa na binadamu hadi leo. Ajabu ni kwamba nyumba hizo zilijengwa kwa udongo, mawe na miti migumu kama mikoko ambayo mingi ingali imara hadi



leo. Kitu kinachovuta macho zaidi ni katika mji huu mkongwe ni mitaa yake. Nyumba hizo zilijengwa katika hali ya kubanana sana kiasi kwamba mitaa yake haiwezi kuruhusu gari kupita na hata baiskeli na pikipiki zililazimika kupita kwa uangalifu sana. Sura hii ya aina yake ya mji huu mkongwe ni moja ya sababu zilizopelekea shirika la elimu la Umoja wa Mataifa liutangaze kama moja ya maeneo ya kihistoria ambayo yanahitaji kuhifadhiwa.


Katika mwambao huo wa bahari nilifurahi sana kuliona jengo maarufu Beit el Ajaib lililojengwa na Sultani Bargash mwaka 1883. Jengo ambalo lina simulizi tele za kila aina. Kwa mfano inaaminika kuwa chini ya kila nguzo ya jengo hilo alizikwa hai mtumwa mmoja. Juu yake likiwa na mnara wenye saa kubwa pia linadaiwa kuwa la kwanza nchini na pengine Afrika nzima kutumia umeme na lifti.


Kando yake nililitembelea pia jengo jingine lililokuwa








likitumiwa kama ngome kuu ya Waarabu. Jengo hilo lenye ukumbi mkubwa na kuta pana lilipanda juu ambako kuna majengo na matunda maalum ya kutumia wakati wa vita. Hata hivyo sisi tulikuta tayari jengo hilo lina maduka, kumbi za wazi za burudani na biashara mbalimbali za sana.


Zanzinbar haina wanyama wengi kama bara. Inaaminika kuwa nchi hiyo haina tembo hata mmoja. Jambo ambalo linawashangaza sana wataalamu wa masuala ya wanyama pori kwani mwaka 1295, msafiri mmoja aliyeitwa Marco Polo aliitembelea Zanzibar kutoa taarifa ya kuwepo kwa mamia ya tembo na wanyama wengine.


Kama tusingekuwa wafungwa tungeshiriki katika ngoma ya ‘mwaka kongwa’ iliyokuwa ikipigwa wakati tukipita eneo la Makunduchi. Tuliishia kuchungulia dirishani tu na kuona wanaume wanavyotoana jasho kwa ndizi na migomba katika ngoma hiyo maarufu ya kila mwaka.


Zanzibar hiyo! Kwa machache niliyobahatika kuyaona, machache niliyopata kuyasikia na kuyasoma sikushangaa pale macho yagu katika tundu nililokuwa nikitumia kuchungulia nje yalipoweza kuona idadi kubwa ya watalii wa Kizungu wakipita hapa na pale katika mitaa, vichochoro na fukwe ya Zanzibar. Nilipata pia kusoma mahala kuwa takribani wageni wapatao 100,000 hutembelea visiwa vya Zanzibar kila mwaka kwa ajili ya shughuli za kitalii.


Gereza la Kiinua Mguu halikuwa tofauti na magereza mengine niliyopata kuyatembelea. Hadithi ilikuwa ileile, chakula kibovu, mlundikano katika selo, chawa na kunguni wakitawala, maradhi ya kila aina na vifo. Tulilala hapo siku tatu kabla ya kupakiwa katika moja ya zile meli zao ziendazo kasi, ambayo ilitufikisha pemba, katika mji wa Wete. Huko








tulielekezwa katika mashamba ya karafuu kuanza kazi.


Nilikuwa nikiifahamu karufuu kwa ladha tu, baada ya kuila sana katika pilau kule Pangani. Aidha, niliifahamu kwa harufu yake tamu puani toka katika marashi ya akina mama wa mjini wanaojiandaa kutoka. Sikupata kufahamu kuwa zao hilo lilikuwa na maajabu zaidi. Kwa mfano, sikujua kama karafuu ilikuwa tiba pia ambayo mafuta yake yalitumiwa kumchua mtu aliyeteguka viungo pamoja na tiba ya meno kwa mwenye maumivu. Nilishangaa zaidi kusikia kuwa karafuu, kwa baadhi ya watu, waliitumia kama sigara wakichanganya na vitu vingine walivyofahamu wao.


Kwa mujibu wa kumbukumbu za kihistoria Sultan Sayyid Said aliyeitawala Zanzibar katika karne ya kumi na nane, alipofika kwa mara ya kwanza nchini humo alishangaa kuona mikarafuu miwili mitatu iliyoota hapa na pale kwa bahari tu ikiwa imestawi vizuri. Wakati huo karafuu likiwa zao hadimu kwa kupatikana katika maeneo machache ya Asia, Sultan huyo alipata wazo. Aliamini kuwa zao hilo lingeweza kuupa nguvu za kiuchumi na umaarufu utawala wake. Hivyo, alilima shamba lake binafsi kama mfano, akapanda miche arobaini na tano. Kisha, akatoa amri kila mtu kulima mikarafuu. Amri ambayo alihakikisha inatekelezwa kwa nguvu zake zote. Hadi anafariki Sultani huyo aliacha tayari biashara ya pembe za ndovu na watumwa ikitishiwa kiuchumi na ile ya karafuu.


Mkarafuu unapendeza kwa macho kama ilivyo harufu yake. Ni mti ambao unakuwa katika rangi yake halisi ya kijani kwa mwaka mzima. Mti huu huenda juu kwa mita kumi hadi ishirini. Maua yake ndiyo karafuu yenyewe. Yako katika sura na maumbile mbalimbali. Maua hayo hupitia rangi mbalimbali kama kahawia, kisha kijani na hatimaye wekundu ambao ndio








huwa dalili ya kukomaa na hivyo huvunwa.


Tulifundishwa yote hayo tukiwa katika uvunaji kazi ambayo ilituweka kisiwani humo kwa miezi mitatu.


Pengine kwa ajili ya ugumu wa usafiri toka kisiwani humo, pamoja na ugeni wetu, hatukushindwa sana kama ilivyokuwa bara na Unguja. Tuliruhusiwa kuchanganyika na wenyeji na, hivyo, kujipatia marafiki wengi wa Kipemba. Hata hivyo, tatizo lilikuwa kuelewana. Ilituchukua muda mrefu kukielewa Kiswahili chao ambacho ama kilichanganyika na kiarabu ama kiliathiriwa na makabila ya asili.


Pemba ilikuwa nyuma kimaendeleo ukiilinganisha na Unguja. Pamoja na kuwa mzalishaji mkuu wa zao hilo la karafuu na mazao mengine, bado wananchi wake wengi zaidi waligubikwa na umasikini. Nyumba zao nyingi zilisikitisha kwa kukosa hata milango, mavazi yao yalikatisha tamaa. Watoto na watu wazima kutembea pekupeku bila viatu ilikuwa jambo la kawaida sana.


Karume amejitahidi. Kila alichokifanya Unguja alikifanya pemba pia. Yale majumba yake marefu yalijengwa pia Wete na mkoani. Wanachi waliishi bila malipo. Hoteli kubwa kama ile ya bwawani pia ilijengwa katika kisiwa hiki kwa kiwango kilekile. Bado wananchi

engi walikuwa taabani na nyuso zao zilionyesha kitu kama kutoridhika au kukata tamaa. Pemba kunani jamani? Nilijiuliza. Kwa kweli, pamoja na uhuru tuliokuwa nao miezi mitatu tulioishi huko niliona kama miaka mitatu ya kuishi katika gereza jingine la aina yake.






















YA ISHIRINI NA TATU


Tumaini Lilirorejea




asaibu ya maisha yanaweza kukupangia jambo ambalo hata hukupata kulifikiria. Mfano mzuri ukiwa wangu mwenyewe. Maishani mwangu


sikukusudia kuwa mhalifu wala sikupata kutarajia kamwe kujikuta nikiishi gerezani kama mfungwa. Lakini ufungwa nao una yake. Ufungwa wangu ulianza kugeuka kuwa utalii.


Mawazo hayo niliyapata tuliporejea toka Zanzibar na kupumzishwa wiki mbili kabla ya baadhi yetu kupangiwa safari nyingine. Mara hii safari yetu ilikuwa ya kueleka Kusini, mkoani Mtwara, ambako tuliombwa kusaidia kazi ya kuchimba mtaro wa kupitisha gesi katika eneo fulanifulani ambayo waajiriwa wa kawaida waligoma kwenda kutokana na ugumu wa mazingira. Sisi, watumwa wasio na wenyewe tulipewa amri tu, ‘Skoch’ ya Mtwara kesho.


Sikupata kufikiria kwenda Mtwara hata mara moja katika ndoto zangu za kimaisha. Mtwara kufanya nini? Wana Mtwara wenyewe walikuwa wanaikimbia. Msamiati wa ‘Wamachinga,’ wale wafanyabiashara vijana, ambao huzunguka na bidhaa zao kila mtaa na kila uchochoro wa jiji la Dar es Salaam, ulizaliwa kutokana na vijana wa Mtwara, pale walipoanza kumiminika mjini baada ya kukata tamaa








vijijini. Walikuja kwa mamia, kutwa wakisaga lami na vumbi la Dar, usiku wakilala kwa dhiki katika vichochoro vya Kariakoo, biashara zao maelfu zikilindwa kama roho zao. Taratibu walianza kuwatishia wamiliki wa maduka, wengi wao wakiwa Wahindi, pale wateja wao walipopunguza kuingia madukani na kuishia kwao. Waliwatishia pia maafisa wa kodi kwani kodi toka kwa wenye maduka zilipungua na kumdai Mmachinga ambaye hujui anaishi wapi, duka lake anatembea nalo, haikuwa kazi rahisi.


Wakati huo ‘Wamachinga’ walichukuliwa kama Wamakua na Wamakonde pekee. Hata jina lao lilitokana na kile kijiji cha Mchinga kilicho Pwani ya Bahari ya Hindi, maili chache toka Lindi. Lakini mafanikio yao tayari yamewavuta Wasambaa na biashara zao za matunda toka Tanga, Wagogo na kahawa zao toka Dodoma, Waha na baiskeli zao toka Kigoma na wengineo. Wote wanafanya kazi za kimachinga na wameafiki jina hilo la Wamachinga pamoja na serikali kuwatafutia majina mbalimbali ya kutia matumaini kama ‘Wajasiriamali, ‘ au ‘Wafanyabiashara wasio rasmi.’


Moja ya sababu zilizofanya nisiote ndoto ya kwenda Mtwara ni zile sifa za ugumu wa safari za kwenda huko. Usafiri wa meli haukuwa na uhakika. Ilisikika habari ya meli moja tu, tena ya mizigo, ambayo ungeisubiri kwa mwezi au miezi kabla ya safari. Meli ambayo ilidaiwa kufurika kupita kiasi na hivyo kuhatarisha maisha ya wasafiri mara kwa mara. Enzi hizo kufikiria safari ya barabara ilikuwa wazimu zaidi. Njia ilikuwa ndefu kuliko ilivyostahili kutokana na ubovu. Yalikuwepo maeneo yasiyopitika, magari ya madereva vichwa ngumu yakizama au kukwama kwa zaidi ya wiki katika tope kabla ya kufikia kivuko cha mto Rufiji na matawi yake.








Pengine kama si kizingiti cha barabara hiyo Mtwara ya leo ingeweza kuwa mfano wa aina yake wa utajiri wa Tanzania, kwani neema ya uchumi ilikuwa imeishukia Mtwara mwaka 1948 Waingereza walipouteua mkoa huu na kongwa Dodoma, maalumu kwa ajili ya kilimo cha karanga. Ekari milioni 325 au kilomita za mraba 13,200 zilitarajiwa kulimwa katika kipindi cha miaka sita na hivyo kuilisha Tanganyika Ulaya nzima karanga na mazao yote yatokanayo na karanga.


Mradi huo ulitengewa dola za Marekani milioni 25. Askari wastaafu laki moja na wakazi wengine tele waliojitokeza kufanya kazi hiyo. Hata hivyo, baada ya jitihada za muda mrefu na kupotea kwa dola milioni 49 zaidi ya zilizotarajiwa kazi ilishindikana. Sababu? Ukosefu wa barabara. Reli iliyokuwepo, ambayo ilitarajiwa kutumiwa kwa usafirishaji wa vifaa na mazao ilichukuliwa na mafuriko ya mto Kinyensungwe. Usafirishaji wa vifaa kama matrekta na mbolea kupitia mto Ruvu nao ulikutana na vizingiti tele; tembo, vifaru na viboko walitishia maisha ya wafanyakazi na hivyo wengi kukimbia. Maradhi ya malaria na matumbo kwa ajili ya maji yasioaminika nako kulichangia.


Jambo jingine ambalo lilisababisha mradi huu kushindikana ni mibuyu. Vifaa vidogovidogo vilivyoweza kufika huko havikuwa na uwezo wa kuing’oa mibuyu mikubwa iliyotanda katika baadhi ya maeneo ya shamba. Si hivyo, baadhi ya mibuyu hiyo ilikuwa na maajabu yake. Baadhi ya mibuyu ilishindikana kutokana na wingi wa nyuki waliokuwa wameweka makazi yao humo, ambao waliwatawanya wakulima hao hadi wakashindwa kufanya kazi yao. Mibuyu mingine ilitumiwa na wenyeji kama matambiko, wasingekubali kamwe








ing’olewe. Mbuyu mmoja ulitumiwa kama gereza kwa ajili ya wahalifu. Huu pia usingeng’olewa.


Hayo na mengine tele yalisababisha tani 2000 tu za karanga zipatikane baada ya miaka tele ya majaribio kabla ya bunge la Uingereza halijatamka rasmi kuuachilia mbali mradi huo mwaka 1951. Kupotea kwa tumaini hilo kuliambatana na kusahauliwa kwa Mtwara, na hivyo kuibuka kwa ukimbizi wa vijana wenye nguvu, kwenda mijini kutafuta maisha kwa ‘Umachinga’.


Hivyo, kugunduliwa kwa gesi, kulikofanywa na kampuni ya Artumas Co. katika mkoa huo ilikuwa neema ya pekee kwa Mtwara na wakazi wake. Lilikuwa tumaini lilirorejea kwa Wamachinga.




* * *


Kwa mujibu wa taarifa zisizo rasmi, ambazo kama wafungwa tulizipata toka hapa na pale wakati tukifanya kazi yetu ya kuchimba



mitaro ni kwamba gesi hiyo iliyogunduliwa ingeweza kutumiwa na mikoa ya Lindi na Mtwara kwa kupikia, kuendeshea viwanda na mahitaji yote ya umeme kwa zaidi a miaka 800.


Taarifa hizo ziliongeza kuwa uamuzi wa serikali ulikuwa kuhakikisha wakazi wa Mtwara, ambao kwa mwaka 2002 walikuwa 1,128,523 wote wanapatiwa fursa ya kuitumia nishati hiyo kwanza kabla haijaruhusiwa kwenda kuwahudumia watu wengine.


Gesi hiyo iligunduliwa Mnazibay, ambako tulipelekwa kufanya kazi. Zilikuwepo pia fununu za nishati hiyo kugunduliwa katika sehemu mbalimbali za mikoa hiyo ya kusini.








Kazi ya kuchimba mitaro hiyo haikuwa rahisi. Kulikuwa na ule wa kupitisha bomba la kuileta gesi hadi Dar es Salaam ambako tuliambiwa kuwa viwanda kadhaa kikiwemo kile maarufu cha Simenti, Wazo, tayari vilikuwa kutumia nishati hiyo badala ya umeme wa TANESO uliozolekea. Umeme ambao ulitegemea zaidi maji ya mvua hivyo, licha ya gharama kuwa kubwa miaka yenye mvua haba ulikuwa matatizo kibao kiasi cha kuanzisha msamiati wa aibu ‘mgao wa umeme.’


Tulifanya kazi yetu kikamilifu, siku tulizopangiwa tulirejeshwa Ukonga, siku zangu za kukaa kifungoni zikifikia ukingoni.


Siku moja bado tukiwa huko Mtwara, nilitembelewa na wazo la ajabu. Kuoa! Sijui wazo hilo lilipenyaje katika kichwa changu kilichofura kwa matatizo na migogoro isiyo na kifani. Mfungwa, asiye na mbele wala nyuma, nawezaje kufikiria kuoa?


Mimi wazo hilo lilinitembelea. Chanzo chake hakikuwa zaidi ya Lulu, msichana wa Kimakua ambaye alitembelea gereza tulilokuwemo akiwa amefuatana na maafisa wenzake wa ustawi wa jamii. Walituweka kikao kwa maelezo kuwa wamekuja kuzungumza nasi kuhusu ya maisha ya uraiani kwani wengi wetu vifungo vyetu vilikuwa vikifikia ukingoni.


Walizungumza mengi. Lakini naapa kuwa hakuna aliyekuwa akiwasikiliza. Lulu, akimeremeta kwa ngozi yake laini ya maji ya kunde, sauti yake ya upole na tabasamu lililosindikiza kauli zake alivutia zaidi ya nasaha zao. Wafungwa wengi walionekana hivyo na walinong’onezana hivyo. Hali ambayo ilidhihirisha zaidi pale tulipopewa wasaa wa kuuliza maswali. Mfungwa wa kwanza alielekeza swali lake moja kwa moja kwa Lulu “Samahani dada Lulu, umeolewa?”








Kila mtu alicheka, ikiwa pamoja na Lulu mwenyewe. “Sijaolewa. Unataka kunioa?” alimjibu na kumtupia


swali pia.


“Huyu akuoe? Atakulisha nini?” alidakia mfungwa mwingine na kuongeza. “Kwanza ni mzee. Kisha hajui kusoma wala kuandika. Kama kuna mume hapa ni huyu mdogo wetu,” alisema akielekeza kidole chake kwangu. “Ni msomi, anazungumza Kiingereza kama Kiswahili. Hata humu ndani amekuja kama ajali tu,” aliongeza.


Sikutarajia kauli kama hiyo. Nilishikwa na aibu kuona kila mtu akinitazama. Lulu Kalenje, kama alivyojitambulisha, alitabasamu kabla hajatamka taratibu, “Naona nimeshapata mchumba. Kwani kaka unaitwa nani?” aliniuliza.


“Petro Kionambali.” Nilimjibu


“Unatoka upande upi wa nchi hii?” aliongeza swali jingine.


“Natokea Kigoma.” “Wewe Muha?” “Haswaa.”


Lulu akacheka tena kabla hajasema. “Sioni kama uchumba wetu utadumu. Watu wa Kigoma hamtuwezi kabisa Wamakua. Tuna tofauti kubwa ya kiutamaduni.”


Nilimwelewa haraka. Nilikuwa nimejifunza mawili matatu juu ya mkoa wa Mtwara na makabila yake kadhaa.


Wageni hao walipoona maswali ya kijelajela yakiongezeka badala ya yale waliyoyakusudia waliaga na kuondoka. Wenzangu walitawanyika. Mie nilibakia palepale kwa muda nikitafakari. Wazo la kupenda na kuoa kwa ujumla lilitokea kusikojulika. Lilijikita kwa muda katikati ya ubongo wangu.


Nilitamani kuoa!








Nilitamani kumwoa Lulu!


Nikamfikiria Lulu, mtoto wa Kimakua. Sikupata kuishi Mtwara. Lakini katika maongezi na tafiti zangu vitabuni nilikuwa nafahamu mengi juu ya mila na tamaduni za Wamakuwa na jirani zao Wayao.


Mtwara, ambayo iko kusini mwa Tanganyika, ikiwa imetengana na nchi ya Msumbuji kwa mto Ruvuma inayo makabila mengi. Makubwa kati yake yakiwa Wamakonde na Wamakua ambao waliingia kutokea Msumbiji. Wayao wanaaminika kutokea Malawi. Hizo zikiwa zile enzi za kuhama kabla ya ujio wa watu weupe ambao walifuatiwa na uamuzi wa uroho na uchoyo uliopelekea kuwekeana mipaka baada ya kupora hiki na kile.


Wamakua na Wayao wanapofikia umri wa miaka kumi hadi kumi na mbili lazima wapitie unyago. Jukumu hilo, huendeshwa na wazee wa kike waliobobea katika masuala ya familia.


Wahusika hulazimishwa kutunza siri yoyote watakayo fundishwa au kuonyeshwa katika mafunzo hayo. Miongoni mwa mafunzo hayo ni jinsi ya kujitunza. Wavivu na jeuri hupewa maneno ya kuwatisha ili waachane na tabia hizo na masuala mengine ambayo somo ataona lazima kuyasisitiza.


Mafunzo hayo hufuatiwa na sherehe za mkesha, ngoma aina mbalimbali kama chimakuani, mtotamto, mselemba na nyinginezo hutumbuiza. Sherehe ambazo huambatana na vinywaji hasa pombe ya mtama ambayo huandaliwa maalum kwa shughuli hiyo.


Yote hayo niliyachukulia kama kawaida. Ambacho nilikiona kizito ni ule utamaduni wao wa kumfanya mtoto mali ya mama zaidi ya alivyo kwa baba. Kwa maana nyingine mtoto








anamsikiliza zaidi mjomba. Ujombani ndio kwao zaidi na ndiko anakokulia.


Kwa falsafa yao mama ndiye hasa anayemjua baba wa mtoto na mama ndiye anayekaa na mtoto tumboni kwa miezi tisa na kumnyonyesha kwa miaka miwili. Baada ya hapo ni yeye anayemlisha na kumvisha hadi anapofikia umri wa kuweza kujitegemea. Hali hiyo husababisha Mmakua au Myao anapooa anahama kwao na kwenda ukweni ambako atapewa shamba na kuonyeshwa mahala pa kujenga ‘mdule’ nyumba zao, ambazo hujengwa kwa fito na udongo paa likiwa la nyasi. Huo huwa



mwanzo wa maisha mapya ya kijana huyo ambaye hata majina ya watoto wake hutolewa na wajomba.


Kwa jinsi nilivyomfahamu baba yangu, mzee Karimanzira Kionambali, sikuiona namna yoyote ambayo angeweza kukubali niingie katika utamaduni wa aina hiyo.


Jingine lililonitisha ni ule utamaduni wao wa kula ‘dagaa changa’ yaani panya. Makabila mengi ya kusini panya ni mlo halali wanaouthamini sana. Unaweza kutengenezewa kitoweo murua, ambacho kitavutia sana, ukala na kushiba bila kujua kuwa unakula panya. Sikuwa tayari kubahatisha hilo pia!


Kwa kheri Lulu! nilivunja uchumba kimoyomoyo. Uchumba ambao hata ulikuwa haujaanza rasmi, mchumba mwenyewe akiwa hata hazifahamu hisia zangu.




* * *


Sitaweza kuisahau tarehe ya kufunguliwa kwangu. Ni tarehe ambayo nimeishi nayo akilini kwa takribani miaka ishirini nikiisubiri kwa hamu. Lakini pale ilipofika na jina langu kutajwa nikiitwa ofisini nilijikuta nikitetemeka kidogo. Wakati wafungwa wenzangu wakinipongeza kwa kutoka








kwangu salama, mimi nilitokwa na machozi. Waliyachukulia kuwa machozi ya furaha. Laiti wangejua!


Nilikabidhiwa vitu vyangu. Suruali mbili, mashati mawili, viatu na kabrasha langu la vitabu. Nililipokea kabrasha hilo harakaharaka na kulikagua. Kitu nilichokuwa na shauku ya kukiona kilikuwepo! Kitabu changu cha benki. Nikakifunua. Akiba yangu ilikuwa kama nilivyoiacha, shilingi 3,500. Nikakitia mfukoni. Nikakabidhiwa tiketi ya treni, daraja la tatu, ambayo ingenifikisha hadi stesheni ya Kigoma. Toka hapo ningejitegemea kufika Kasulu na hatimaye kijijini kwetu.


Nilikuwa mgeni sana Dar es Salaam. Toka nilivyofika kwa muda ule mfupi na akina Leakey sikupata kurudi tena. Sikuwa na wenyeji wala rafiki ambaye angeweza kunipokea. Hivyo, pale lango la gereza lilipofunguliwa nami nikaruhusiwa kutoka sikujua toka hapo ningeelekea upande gani wa dunia.


Kweli Mungu si Athumani. Wakati bado nashangaa hapo nje gari la mkuu wa gereza lilitokea. Aliponiona akaniita. “Hongera,” alisema “Nategemea hutajiingiza tena katika jambo lolote la kinyume cha sheria ambalo linawea kukurejesha hapa.” Baada ya maneno hayo aliutia mkono wake mfukoni na kuuchomoa ukiwa na noti tatu za elfu kumikumi. Shilingi 30,000! Sikuyaamini macho yangu.


“Mbona nyingi sana mzee?” nilimuuliza


“Nyingi?” alijibu akicheka. “Hazikutoshi, lakini zitakusadia.” Akalitia gari lake moto na kuondoka zake hata kabla sijamshukuru kikamilifu.


Kwa maelekezo ya wapita njia nilifika kituo cha mabasi ya mjini wenyewe waliyaita ‘daladala’. Nikauliza basi la kuelekea stesheni ya treni, nikapanda, kondakta, kijana mdogo mweye lugha ya kihuni alikuwa mtu wa kwanza aliyenipa mshangao








wangu wa kwanza. Ni pale aliponiomba nauli nami kumpa moja ya zile noti nilizopewa na mkuu wa jela. Nilihesabu kwa makini chenji alizonipa. Alikata shilingi mia mbili.


“Nauli mia mbili?” nilifoka.


“Kumbe ngapi?” alinijibu kwa swali vilevile. Alinitazama kwa makini. Nywele zangu zilizoanza kuingia mvi ziliashiriwa ovyoovyo. Suruali yangu iliyopauka ilikuwa pana kiunoni, fupi miguuni ikinifanya nionekane kama moja ya vile vikatuni vinavyochorwa magazetini, sura yangu pia, nadhani ilionyesha ugeni na mshangao kwa kila nilichokiona, wingi wa watu wa magari, wingi na ukubwa wa majengo na kadhalika.


“Au umetoka pale mjomba?” Yule kondakta alihoji. “Pale wapi?” nilimuuliza


Pale mtakuja, ukumbi wa wanaume,” alijibu akielekeza mkono maeneo ya gereza.


“Unauliza jibu?” abiria mmoja alidakia.


Sikuwajibu. Hofu niliyokuwanayo juu ya maisha ya uraiani ilianza kunirejea. Shilingi mia mbili kabla sijaingia gerezani ilitosha kumsomesha mtoto wa mwaka mzima. Wakati huohuo kodi ya chumba kwa mpangaji ilikuwa senti ishirini, shati senti kumi. Nauli halali ya basi kama hilo isingezidi senti tano.


Kumetokea nini? Nilijiuliza. Tulipita Tabata, tukaingia barabara ya Mandela na kuifuata hadi Buguruni ambako tulichukua barabara ya Pugu kueleka mjini. Barabara hiyo ikiwa barabara pekee inayoelekea uwanja wa ndege wa Julius Nyerere magari yalikuwa tele barabarani yakishindana kwa kasi. Aidha, barabara hiyo ilikuwa katikati ya viwanda mbalimbali vilivyotapakaa hadi Chang’ombe na Vinginguti, hali iliyozidi kuipa purukushani za aina yake. Mwendo wa kasi








wa magari hayo na majonjo ya dereva wetu utadhani hana roho vilinitia roho mkononi hadi tulipofika kituo cha stesheni ambapo nilishuka.


Mshangao wa pili ulinisubiri nilipofika stesheni. Nilikuta pamefurika watu, wengi wao wakiwa na mizigo tayari kwa safari. Lakini nilipofika dirisha la tiketi kwa nia ya kuithibitisha tiketi yangu niliulizwa swali ambalo sikutarajia.


“Unataka kuondoka lini?” “Leo.”


“Haiwezekani. Nafasi zimejaa. Labda ufanye booking ya siku nyingine.”


“Haya, nipe tiketi ya kesho.” “Kesho hakuna treni.” Sikuelewa. “Kwa nini?”


“Treni ni mara tatu kwa wiki,” alinifafanulia. “Na ratiba yangu hapa inaonyesha kuwa daraja la tatu limejaa hadi baada ya wiki tano hivi.”


Sikuamini kama nilikuwa nimemsikia vizuri. Treni inasafiri kwenda bara mara tatu kwa wiki! Treni hiyohiyo ambayo wasafiri ni wengi kiasi cha kuifanya ijae hadi kwa wiki tano zijazo! Treni hiyohiyo ambayo ilikuwa ikisafiri kila siku na abiria wakichagua kiti cha kukaa!


“Kwani kumetokea nini?” nilimuuliza karani huyo.


Alinitazama kwa macho ya mshangao kana kwamba nina pembe ya faru usoni. Nadhani aliishuku hata akili yangu. Kwani badala ya kunijibu alifunga dirisha lake.


Kijana mmoja aliyekuwa pembeni akifuatilia majibizano yetu alinivuta kando na kuniuliza “Unataka tiketi ya kuondoka leo? Toa kitu kidogo tu utasafiri.”


“Tiketi ninayo.” Nilijibu nikimwonyesha.








“Sasa tatizo lako nini? Treni ikifika panda. Hakuna


atakayekushusha. Mradi uwe tayari kwenda wima.” “Wima! Toka Dar es Salaam hadi kigoma!”

Niliamua kuufuata ushauri wa kijana huyo. Bado zilikuwepo saa sita kabla ya treni kufika, masaa mawili kabla ya muda wa kuondoka. Nikaamua kuutumia muda huo kutafuta benki ambayo nilikuwa nimefungua akaunti yangu.


Ilikuwa kazi nyingine ngumu. Mji ukiwa umepanuka sana, majengo mengi yakishindana kwenda angani, huku watu wakiwa tele na pilikapilika kibao ilinichukua muda kabla ya kumpata mtu aliyenielekeza hadi kuifikia benki hiyo.


Afisa niliyeelekezwa kwake alinipokea kwa heshima zote katika chumba chake kidogo chenye hewa safi iliyokuwa ikitoka katika kiyoyozi. Hewa ambayo iliniburudisha sana kutokana na jasho tele lililokuwa likinitoka. Akapokea kitabu changu na kukitazama kwa mshangao kidogo. Nadhani kwa umri wake hakupata kuona aina hiyo ya kitabu, kwani vilishabadilishwa mara nyingi. Hata hivyo, alipoichezea kompyuta yake kwa muda mrefu aliliona jina langu.


“Petro Kionambali sio?” akauliza. “Ndiyo,” nilimjibu kwa matumaini. “Mbona huna pesa?” aliniuliza tena


Sikumwelewa, “Kwa vipi? Mara ya mwisho nilikuwa na elfu tatu.”


“Ni kweli kabisa,” alijibu. “Miaka ipatayo ishirini na mbili akiba yako ilikuwa elfu tatu. Halafu ukapotea. Gharama za kutunza akaunti yako na kushuka kwa thamani ya pesa kumefanya uwe huna pesa kabisa. Kwa kweli, benki inakudai.”


Ulikuwa mshangao wangu wa tatu katika siku yangu ya kwanza uraiani. Nilihisi naishiwa nguvu, miguu na mikono








ikitetemeka. Pamoja na kiyoyozi jasho jembamba lilianza kunitoka. Kwa sauti dhaifu niliuliza, “Unasema? Sijakuelewa… Nilitarajia fedha zangu ziwe zimeongezeka sana. Unajua wakati ule fedha zile zingenitosha kununua magari hata mawili na kujenga nyumba?”


“Ni kweli kabisa,” alinijibu. “Tatizo lilikuwa lako wewe. Benki ikaendelea kukata gharama zake, fedha zikaendelea kushuka thamani. Kibenki elfu tatu ni elfu tatu tu. Ungekuwepo ukazitumia zingezalisha faida. Kwa bahati mbaya ulipotea. Kwani ulikuwa wapi mzee?”


Sikumjibu. Nilijikongoja kuinuka. Nikapepesuka. Nikajikongoja tena kutoka nje ya ofisi hiyo, macho yakiwa hayaoni vizuri, miguu ikiwa haina nguvu.




.
























YA ISHIRINI NA NNE


Dar jiji la Raha na Karaha




ar es Salaam niliiona chungu. Watu, majengo, magari na kila nilichokiona mbele yangu kilinitisha na kuniogofya. Ndiyo, mji ulikuwa


mzuri, uking’ara kwa usafi. Barabara zilimeremeta kwa usafi, magari yakipendeza ubora na thamani. Watu pia walipendeza mitaani.


Wengi wao walivaa mavazi ya bei, waliharakisha kwenda hapa na pale huku nyuso zao zikiwa na dalili za matumaini kinyume cha ilivyokuwa miaka ya nyuma.


Yote hayo niliyaona na yalinivutia, lakini bado Dar es Salaam niliiona chungu. Ilikuwa baada ya lile pigo la mwisho pale benki. Pigo ambalo liliniacha taabani, nusu hai nusu maiti.


Sikujua nilitoka vipi pale benki hadi stesheni ya reli. Sijui ilikuwaje hata nikafika huko bila kugongwa na moja ya magari tele yaliyotapakaa barabarani kama siafu. Mradi nilijikuta mbele ya stesheni, macho yangu yakikodolea macho saa kubwa ya kwenye mnara. Ilionyesha kuwa bado kulikuwa na saa kama tano kabla ya treni kufika! Saa tano, ambazo niliziona kama miaka mitano! Sikuwa na jinsi. Ilibidi niendelee








kusubiri. Kila dakika moja ya kuendelea kusubiri ilinitesa kama msumari wa moto moyoni.


Mara kwa mara, nilitoa zile senti zangu nilizopewa na mkuu wa gereza na kuzihesabu. Nilikuwa nimezipunguza kwa nauli ya daladala. Mia moja nyingine nililazimika kuzitumia kwa huduma ya choo! Nilikuwa na kiu lakini kila bomba nililofungua halikutoa maji. Baadhi ya ‘wamachinga’ walikuwa wakiuza maji ya chupa. Chupa ndogo mia tatu, kubwa mia saba hadi elfu moja. Maji ya kununua? Maji ambayo utoto wangu wote nimeyachezea katika mito, katika maziwa na hata baharini! Niliamua kujikaza kisabuni.


Nilikuwa na njaa vilevile. Lakini sikuthubutu hata kuuliza bei ya chakula. Nilijua ingebomoa zaidi visenti vyangu ambavyo sasa ilikuwa akiba yangu pekee maishani mwangu. Akiba ambayo ilikuwa lazima inifikishe nyumbani kwetu. Nikaamua kuivumilia njaa vilevile, nikifumbia macho watu wanaokula na kuizibia pumzi harufu tamu ya maakuli.


Saa zilikuwa haziendi. Nikaamua kupitisha muda kwa kutembeatembea mitaani. Nilifuata barabara ya Samora. Macho hayana mipaka, yangu yalipenya vioo vya maduka mbalimbali na kushuhudia vitu vilivyofurika madukani. Vifaa vya elekrtroniki, kama televisheni, deki, dvd, projekta na vinginevyo vilikuwa tele katika sura na bei mbalimbali. Nguo, viatu, pochi za kinamama na vinginevyo vilikuwa tele. Duka moja lilibandika bei kwenye bidhaa zake, viatu 120,000/= suti 550,000/= pochi 85,000/=! Sikuelewa. Sikuelewa zaidi pale nilipoona maduka hayo yakiwa yamejaa watu wakinunua vitu hivyo kwa fujo kana kwamba wana viwanda vya kuchapa noti. Macho yangu yalivutwa pia na watu, hasa wasichana.


Mavazi yao yalinitisha. Baadhi walivaa nguo fupi sana,








mapaja wazi, sehemu kubwa ya tumbo nje huku wakitembea hadharani bila wasiwasi wowote. Baadhi ilikuwa vigumu kujua kama walikuwa wasichana au wavulana kwa suruali zao za jeans. Fulana na kofia kwenye vichwa. Kitu kingine kilichonishangaza ni kuona wasichana wengi walivyofanana. Karibu wote walikuwa weupe! Karibu wote walikuwa na nywele za kizungu! Wengi midomo yao iling’ara kwa rangi nyekundu kama ndege! Wengi walinukia manukato makali ambayo siku za nyuma ungeamini kuwa umepishana na jini! Sikuelewa hali hii hadi nilipofikia duka moja lililokuwa likiuza aina mbalimbali za nywele kama nilizoona kwenye vichwa vya akina dada na kila aina ya vipodozi! Kumbe!


Wavulana wengi nao walinikatisha tamaa. Walivaa jeans zao ambazo zilichakaa au kuchakazwa makusudi, sweta au fulana zenye picha za wacheza sinema wa Marekani kama Rambo na

eb 3, 2021

Thread starter

Add bookmark

#175

schwarznegger, huku wakiwa wamefunika vichwa vyao kwa kofia au vitambaa vyenye nembo za bendere ya Marekani. Baadhi yao walisuka nywele zao, baadhi walivaa hereni! Ilikuwa vigumu kujua kuwa vijana hao walikuwa Watanzania au Wamarekani weusi hadi pale utakapowasikia wakizungumza Kiswahili. Lakini Kiswahili hicho nacho kilikuwa na manjonjo yake. Kwa kweli, kilistahili kuitwa Kiswaengilish kwa jinsi kilivyochanganywa maneno ya Kiingereza na hata ya mitaani ambayo watu kama Shaaban Robert wangefufuka, wangeweza kuangua kilio.


Wakati huo nilikuwa tayari nimeloa chapachapa kwa jasho. Joto la hapa, mara nyingi linatisha. Nilitamani kununua leso kama nilivoona wengine wakifanya lakini sikuthubutu. Shilingi mia tatu za kulipia kitambaa hicho niliziona kama milioni. Nikawa nikitumia kiganja au kiwiko cha mkono walao








kupunguza jasho la usoni ili niweze kuona niendako.


Wingi wa watu lilikuwa tatizo jingine. Mara kwa mara, niligongwa na mtu au kupigwa kikumbo kilichofanya nikaribie kula mweleka. Nilipogeuka kumtazama mtu niliyegongana naye alikwishakwenda zake bila hata kugeuka nyuma. Hiyo ilinifanya nikumbuke kile nilichosoma nikiwa gerezani juu ya kasi ya ongezeko la watu jijini hapa. Kwamba mwaka 1925 mji huu ukiitwa Mzizima ulikuwa na watu 30,000 tu. Leo unatisha.


Nilifika katikati ya mji wa Dar es Salaam. Pale nilipopita miaka mingi iliyopita na kusimama mbele ya sanamu ya yule Mjerumani machachari Bismarck akiwa na bunduki mkononi kaielekeza baharini. Sanamu hiyo haikuwepo tena badala yake ilijengwa sanamu ya askari mweusi kama mkaa, ikiwa na silaha vilevile kuashiria tulivyopigana na kufa kwa vita ambavyo havikuwa vyetu. Niliitazama kwa muda kabla ya kuendelea na safari yangu, taratibu hadi nilipoifikia bustani ya Ikulu. Miti mingi ya asili ilikuwemo kama nilivyoiona mara ya mwisho. Hata hivyo, nilihisi kuwepo kwa aina fulani ya upungufu. Nini kilichopungua? Nilijiuliza. Nikajibiwa na ukimya mkubwa wa eneo hilo. Ni ukimya huo ulionipa jibu. Zile kelele za wanyama na ndege mbalimbali, hasa tausi, hazikuwepo tena. Tausi wale, ambao mara ya mwisho walinivutia sana kwa jinsi walivyoipamba bustani hiyo kwa maringo na ulimbwende, mara kwa mara wakitoa sauti zao nzuri na kuifumua mikia yao iliyoficha kila aina ya rangi hawakuwepo tena. Walienda wapi? Nilijiuliza bila matarajio ya jibu lolote.


Nikashuka kilima cha Ikulu na kufika Pwani ya Magogoni. Kigamboni ilikuwa upande wa pili wa bahari kama nilivyoiacha. Lakini, sasa, badala ya kuvuka kwa mitumbwi ya makasia kulikuwa na chombo maalum ambacho kilipakia








watu, magari, mazao na hata mifugo yao na kuwavusha upande huu au ule. Nilitamani kuvuka katika kupoteza muda. Lakini nilipoambiwa kuwa ningelazimia kulipia, niliachana na mpango huo.


Nikalisogelea soko la mnada wa samaki. Biashara ilikuwa ikiendelea kama kawaida. Kando kidogo, akina mama walioitwa ‘mama ntilie’ walikuwa kazini wakitoa huduma ya chakula kwa haraka na kwa bei nafuu. Wakati huo tayari natetemeka kwa njaa, chango likinguruma kudai chochote, nilishindwa kujizuia zaidi. Nikaingia katika banda la mmoja wao na kuomba wali kwa samaki. Nilikula wali mtamu sana wa nazi ambao sikupata kuula kwa takribani miaka ishirini. Hata kabla sijakitafuna kichwa cha samaki wangu mmoja kunguru tele waliozagaa huko na huko jiji zima alitua ghafla na kukipokonya. Huyoo, akapaa hadi juu ya paa na kuanza kukila huku kunguru wenzake wakimshangilia. Watu wawili watatu walicheka. Mama ntilie wangu akaniongeza mboga, nikaendelea kula nikimlaani kunguru yule.


Nikakumbuka kusoma mahala, ama gazetini ama kitabuni, juu ya tatizo la ndege hao waliozagaa mjini Dar es Salaam, kwamba wameondokea kuwa kero ya kitaifa; wanaiba kila kinachoibika ikiwa pamoja na nyaya za umeme au vifaa vingine vya kiufundi. Kwamba ndege hao waliletwa nchini, kupitia Zanzibar mnamo miaka ya 1900 na wakoloni wa Kiingereza kwa kusudi la kuwafanya wasaidie usafi kutokana na tabia yao ya kula mabaki ya chakula, mizoga na takataka nyinginezo. Lakini hadi kufikia mwaka 1930 walijifanya ndege wa mjini ambao ni nadra sana kuonekana vijijini.


Nikauliza saa. Nilikuwa nimetumia saa moja na robo tu toka nilipoondoka stesheni. Bado nilikuwa na muda wa








kutosha. Nikaamua kutembea tena, safari hii nikielekea Kariakoo. Kinyume na safari yangu ya mwisho mjini hapo sikuona pori wala jani. Kisutu ambayo zama zile nusu yake ilikuwa pori, fisi wakirandaranda kutafuta chochote, sasa ilikuwa sehemu ya mji iliyotapakaa watu na majengo hadi upeo wa macho. Kilabu cha askari wa zamani kilikuwa pale. Lakini sasa kilijengwa jengo bora zaidi la ghorofa likiwa na wapangaji tele wenye shughuli zao. Ukumbi ulikuwa pale lakini haukuwa na pilikapilika zile za zamani. Ama wanachama wengi walikuwa wamekufa kwa umri mkubwa ama wamekata tamaa.


Kariakoo nayo ilikuwa muujiza mwingine. Pengine soko jipya lililojengwa juu ya lililokuwa handaki la kivita enzi za Mjerumani lilikuwa limevuta watu toka kila pembe ya mji na nchi ama Mungu alikuwa amedondoshea neema eneo hilo. Si haki kabisa kusema watu walikuwa wengi, bali walifurika! Mitaa ya Kongo na Msimbazi ilikuwa haipitiki. Kila mmoja akiwa na pilikapilika zake. Nje na ndani ya soko ndiyo ilikuwa kabisa. Kupumua peke yake ilikuwa shida, achilia mbali kutembea.


“Dingi vipi… mbona unashangaashangaa? Ambaa tupite,” kijana mmoja alinifokea baada ya kunipiga kikumbo.


Nikageuka kumtazama.


“Unashangaa nini? Kashangae feri, ambako shilingi inazama meli inaelea. Siyo hapa.”


Aliongeza.


Sikumwelewa kabisa. Nikajikokota kuondoka.

Ilikuwa kazi kubwa kujichoropoa toka katika umati huo na kuifuata barabara ya Uhuru hadi stesheni ambako niliamua kukatisha moja kwa moja na kuisubiri treni.


Nilijiunga na wasafiri wenzangu, wengi wao wakiwa na








mizigo na familia zao. Mmoja kati yao, aliyekuwa na mizigo mingi zaidi alikuwa msichana wa Kizungu. Mwembamba, mwenye pua ndefu na sura ya utulivu. Alikuwa peke yake akilinda mizigo yake kwa makini. Hali hiyo ilinifanya mie pia nizikumbuke pesa zangu. Nikatia mkono wangu mfukoni kwa nia ya kuzipapasa.


Mfuko ulikuwa mtupu! Nilishtuka kama niliyeguswa na waya wa umeme. Nikainuka na kukagua kila mfuko wangu. Hamkuwa na kitu. “Nimeibiwa!” nilisema kwa sauti huku nikitetemeka. Msafiri mmoja aliyekuwa akisubiri usafiri kama mimi aliniuliza taratibu, “Umeibiwa nini mzee?”


“Pesa,”” nilimjibu. “Nyingi?”


“Hapana za kutosha lakini. Zilikuwa pesa zangu pekee.”


“Pole sana. Alisema. Umeibiwa hapa?” “Hapana. Bila shaka ni Kariakoo.”


Alinishangaa, “Ulienda Kariakoo? Kule hakufai kabisa.” Nikamkumbuka yule kijana aliyenipiga kumbo na kisha kuniita ‘Dingi’. Nilihisi hatukugongana naye kwa bahati mbaya. Alikusudia. Ni yeye aliyeniibia au kuandaa mazingira ya kuibiwa kwangu. Sasa sina hata shilingi moja. Sina kitu chochote ninachoweza kuuza nipate walao nauli ya kunitoa


Kigoma mjini na kunifikisha Kasulu!


Badala ya kulia niliangua kicheko. Kwa jinsi nilivyovaa, nilivyochakaa kwa jasho na vumbi, nadhani watu waliokuwa wakinitazama walishuku iwapo nilikuwa na akili timamu au la. Sikujali. Niliendelea kucheka, peke yangu. Kilikuwa kicheko cha uchungu, ambacho baadaye kiligeuka kuwa kilio. Nilijificha katika uchochoro mmoja na kuruhusu machozi kunitririka.








Muda wa treni kufika ulikaribia. Kila mmoja alikaa tayari kwa vita ya kuwahi kuingia ndani. Lakini pale mmoja wa makarani wa TRC alipouendea ubao wa matangazo na kuandika kitu kwa chaki kila mtu alipigwa na butwaa. Mimi nilichanganyikiwa zaidi, mara baada ya kuusoma ujumbe ule. Yule mwanamke wa kizungu, ambaye bila shaka hakujua Kiswahili vizuri alinisogelea na kuniuliza kwa Kiswahili chake


kibovu, “Hiyo maana yake gani?”


Nikamfahamisha kwa Kiingereza. “Wanasema leo hakuna treni, hadi kesho.”


Yeye pia alipigwa na butwaa. Akanikazia macho ya mshangao kabla hajauliza tena, “Kwa sababu gani?”


“Sijui. Hawakuandika sababu.” “Na hiyo kesho, ni saa ngapi?” “Hilo pia hawakueleza,” nilimjibu.


Mama wa watu alitazama lundo la mizigo aliyokuwa nayo, akatazama kundi la watu waliokuwa pale, ambalo hakuweza kupambanua nani alikuwa msafiri kweli nani kibaka; akazidi kuchanganyikiwa.


Minong’ono mingi ilikua ikiendelea. Habari zilikuwa zimevuja. Treni ya mizigo ilikuwa imeanguka huko Kilosa na kufunga njia. Jitihada za kuinua na kisha kurekebisha uharibifu uliotokea zisingekamilika hadi kesho yake. Hivyo, hakukuwa na namna ya kuondoka hadi jioni ya kesho, kama tutakuwa na bahati.


Nilimfahamisha hayo yule mama wa Kizungu. Kiasi alielewa. Akanishukuru. Nikamwona akihangaika kutafuta namna ya kuondoka na vitu vyake vingi. Masanduku, maboksi na vikorokoro tele ambavyo hata sikuweza kubuni vina nini ndani. Nikajitolea kumsaidia. Tulibeba mizigo hiyo kwa taabu hadi chini ya mnara wa saa ambapo alizungumza na dreva








mmoja wa teksi, wakakubaliana. Tukapakia vitu hivyo katika gari hilo.


“Wewe je? Utalala wapi?” Aliniuliza wakati akijiandaa kuingia ndani ya gari hilo.


“Nitafanya maarifa.” Nilimjibu


Alinitazama kwa muda kabla hajaifungua pochi yake ndogo na kutoa noti ya shilingi elfu kumi ambayo alinikabidhi. Katika hali ya kawaida nisingeweza kupokea fedha hizo, lakini kwa hali niliyokuwa nayo na shida ingekuwa dhambi kubwa kuzikataa. Nilimshukuru mara mbilimbili, kimoyomoyo nikimshukuru mara elfu na mbili. Ilikuwa kama nimepata milioni kumi!


Nikarudi stesheni. “Maarifa” niliyokusudia kufanya yalikuwa ni kuupitisha usiku hapo stesheni, ikiwezekana nilale juu ya viti vyao vya mbao, kuisubiri kesho. Sikuwa na bahati hiyo. Mara tu nilipopata kiti na kujipumzisha alikuja askari mmoja wa shirika hilo na kututangazia kuondoka hapo mara moja, utadhani tulipenda kuwa hapo. Tulipositasita walianza kutuswaga kama mifugo. Hatukuwa na namna zaidi ya kuinuka na kuondoka.


Niende wapi? Nilijiuliza. Wakati huo usiku ulishaingia, yapata saa mbili hivi. Tukio la mchana kule Kariakoo lilikuwa limenitia hofu kubwa ya kuibiwa tena. Kutembea usiku kucha pia kuliniogopesha. Hatari elfu moja na moja zingeweza kunitokea; ningeweza kupigwa na majambazi kwa kufikiriwa kuwa nina pesa; ningeweza kukamatwa na polisi na kurudishwa jela kwa kosa la uzuluraji. Ningeweza hata kuuawa na walinzi wa mabenki na majumba mengine kwa kisingizio cha kujaribu kuiba; na kadhalika na kadhalika.


Wakati nikijiuliza hayo nilikuwa nikirandaranda mitaani kwa hofu ya kukaa mahala pamoja kwa muda mrefu








na kushukiwa. Nilishangazwa na utulivu wa mji, tofauti kabisa na mchana. Watu wengi walijaa katika vituo vya mabasi wakipigania kurudi makwao, pembeni mwa mji. Katikati ya mji watu wengi niliowaona walikuwa Wahindi. Walipita katika magari yao au kuketi katika sehemu zinazotengenezwa vinywaji na kuku choma wakitumia. Nasikia wao, kwa ajili ya rangi zao na imani ya watu wengi kuwa wana fedha nyingi zaidi ni waoga wa kuishi uswahilini. Wako tayari kuishi mtu na mkewe na mama na na baba na watoto sita katika kijumba chenye chumba na sebule badala ya kwenda kando ya mji ambako wangechanganyika na Waswahili.


Niliacha barabara ya uhuru, nikaifuata ya Bibi Titi. Nikaifikia bustani ya Mnazi mmoja. Nikashangaa kuona kundi la watu, wakubwa kwa wadogo wakiwa humo ndani. Baadhi walikuwa wakipika kwa kuni.

Nikawasogelea kwa matumaini ya kupata hifadhi ya kupumzika hadi kesho. Haikuwa. Kumbe hawa walikuwa ombaomba, jamii mpya iiliyokuwa imeibuka na kujengeka nchini. Wakati wazazi walikuwa na tatizo moja au jingine, ama katika viungo ama katika mfumo wa kufikiria, watoto walitumiwa zaidi katika kuomba wapita njia, hasa wenye magari. Watoto hawa hawakuwa na mipango wala matumaini ya kwenda shule. Hivyo, walikuwa wakiandaliwa kuwa ombaomba wazoefu au majambazi sugu wenye hasira na maisha. Zaidi ya kuwakamata mara kwa mara na kuwarejesha vijijini, ambako walikaa siku mbili tatu na kurudi zao mijini, hakuna jitihada kubwa ya dhati iliyofanyika kuondoa tatizo hili linalozidi kuchanua.


Jamii hiyo haikuonyesha dalili za kunitaka katika kundi lao. Hata salamu zangu hazikujibiwa. Badala yake walinong’ona wenyewe kwa wenyewe kabla ya kuanza kutafuta silaha zao, fimbo, mawe na hata upanga. Sikusubiri








kufukuzwa. Nikajiondoa harakaharaka na kuendea kituo cha mabasi kilichokuwa na watu tele.


Naweza kupata wapi sehemu ya kulala? Nilimuuliza mtu mmoja aliyekuwa akisubiri basi.


Alinitazama kwa macho ya dharau, bila shaka akinichukulia kama kibaka aliyekuwa akitafuta namna ya kujichanganya ili baadaye apore chochote kinachoporeka.


Mtu wa pili alinijibu kwa kunielekeza kwa mkono. Nikainua uso wangu. Jengo kubwa lililopaa angani kwa takribani gorofa nane lilikuwa likimeremeta mbele yangu kwa nuru ya rangi mbalimbali toka katika vioo. Maandishi yenye maremborembo yalikuwa yakicheza kwa kuwaka na kuzimika, kila herufi kwa wakati wake na kusomeka, Peacock hotel.


Nikamtazama jamaa yule na kumcheka kimoyomoyo, jambo ambalo hakunielewa. “Kama haikufai,” alisema. “Ziko nyingine tele. Zipo za shilingi 500,000 kwa siku. Ziko za 100,000/= na hata zile za 20,000/=. Ni mfuko wako tu. Unaweza kulala Sheraton, unaweza kulAla Kilimanjaro hotel au ukitaka Holiday Inn. Kama unataka hoteli za ufukweni nenda zAko Kipepeo Kigamboni, nenda Kunduchi au Bahari. Ziko tele…”


Nikabaini kuwa nanidhihaki. Nikasogea na kumnong’oneza karibu kabisa na sikio lake, “Natafuta hoteli za chumba cha shlingi elfu moja au mbili, sio zaidi.”


Akacheka. Kisha akasema, “Hizo pia nyingi tu. Utazipata Manzese kwa mfuga mbwa, Buguruni kwa Bibi Tarabushi au hata Mwananyamala kwa Mama Zakaria. Ukiwa na bahati hata Mapipa utapata.”


“Ni wapi huko?” nilimuuliza. “Panda basi, nitakuonyesha.”


Nilimfuata ndani ya basi. Tukaketi kiti kimoja. Alishajua








kuwa nilikuwa mgeni wa mji. Hivyo, alinipa hadithi moja baada ya nyingine juu ya mji na vitongoji vyake.


“Unajua kwa nini panaitwa Mapipa?” alitaja. “Zamani palikuwa na vibanda vilivyojengwa kwa mapande ya mapipa juu na chini. Mapipa hayo ni yale yaliyotupwa wakati wa ujenzi wa barabara ya Morogoro. Yalikuwa na soko kubwa pale Mapipa.


“Lakini wakati ule Magomeni haikuwa kama hii ya leo. Mitaa yote ilikuwa na lami. Umeme uliwaka kila mtaa. Mifereji ya maji machafu ilikuwa imejengwa na inahudumiwa vizuri. Leo hii kila kitu kimekufa. Maji machafu yanamwagika hadi barabarani. Taa zimekufa, lami imekufa. Hata mabomba hayatoi maji.”


“Nini kilitokea?” nilimuuliza. “Sijui,” alijibu


Pamoja na maelezo yake nilikuwa nikishangazwa pia na ukubwa wa mji wa Dar es Salaam. Toka katikati ya mji hadi tunafika Magomeni isipokuwa jangwani ambako wakati wa masika hufurika maji, sikuona pori. Mji ulikuwa umeungana, nyumba kwa nyumba, mtaa kwa mtaa. Wakazi walikuwa hawalali. Karibu kila mtaa niliona baa mbili au tatu, zikiwa zimechanganyika na makazi ya watu, makelele ya muziki yalishindana kwa sauti.


“Hivi hakuna biashara nyingine Dar es Salaam?” nilimuuliza mwenyeji wangu huyo.


“Kwa nini?”


“Naona baa kila mahala.”


Pombe ndiyo bidhaa inayotoka kuliko nyingine,” alinijibu. “Maduka mengi ya vitabu yamefungwa. Watu hawanunui isipokuwa kile kilicholazimishwa na Wizara ya Elimu. Maduka ya madawa pia yameanza kukosa wateja. Watu hawana uwezo








wa kununua dawa dukani wala hospitalini. Mtu anaweza kufa hata miguuni mwa daktari, kama hana pesa za dawa hakuna matibabu.”


“Kwa nini?” Nilimuuliza kipumbavu. “Sijui,” alinipa jibu lilelile nililostahili.


Karibu kila kituo cha basi tuliwaona wasichana wadogowadogo waliovalia mavazi yao ya kutisha, wenyewe wakiyaita ya kisasa; wakiwa wamesimama. Hawakupanda basi lolote wala kuonyesha kuwa na haraka yoyote, usiku mwingi kama huo. Niliwatazama kwa mshangao.


Mwenyeji wangu aliusoma mshangao wangu, “Changudoa!” akasema.


“Nini?”


“Wale pale! Wanajiuza. Tunawaita Changudoa,” alifafanua.


“Si nasikia kuna maradhi hatari yanayoitwa UKIMWI?” “Naam,” alinijibu. Tena omba kusikia usiombe kuuona


kwa macho. Lakini kwa wale, UKIMWI ni ajali kazini!” Sikuelewa. Nikanyamaza.


Tulifika Manzese. Tukashuka kituo cha karibu na daraja pekee la angani, lililoikata barabara ya Morogoro toka kulia hadi kushoto kupunguza ajali za barabarani ambazo niliambiwa ziliua waenda kwa miguu kwa wingi kuliko UKIMWI au malaria.


Nilielekezwa kuelekea kushoto. Kona moja, uchochoro; kona ya pili; uchochoro. Mara tukamezwa na kiza kizito. Bila msaada wa nuru hafifu toka katika vyumba vya wakazi wa eneo hilo nadhani hata mwenyeji wangu angeweza kupotea. Nilimfuata katika vichochoro hivyo, vilivyobana na kugubikwa na uchafu mwingi. Mara kwa mara tulikanyaga dimbwi la tope.








Mara mbili tatu tulikurupusha wanyama wadogowadogo ambao mimi nilidhani ni paka lakini mwenyeji wangu akaniambia, panya!


“Mbona wanene vile?” nikauliza.


Wanakula na kushiba. Manzese hii mjomba,” alijibu. Tulizidi kuingia ndani. Mwenyeji wangu alitembea haraka akipenya hapa na kutokea pale. Nilianza kuogopa. Kwanza, nilihisi kuwa hajui tunakokwenda. Pili, nilianza kumshuku kuwa huenda alikusudia




kunitendea ubaya. Nikatamani kugeuka nirudi nilikotoka. Hata hivyo, hofu ya kupotea na kupatwa na mabaya zaidi ilinizuia. Badala yake nikamuuliza taratibu, “Mbona hatufiki?”


Aligeuka na kunitazama. Aliisoma hofu katika macho yangu. Akacheka. “Hofu ya nini?” aliuliza baadaye. “Hapo ulipo hata laki huna, achilia mbali milioni. Nataka kukusaidia upate mahala pa kulala, kwani unaonekana kuwa unahitaji msaada. Nikikuacha utapigwa na vibaka na kuvuliwa hata nguo ulizovaa.”


Nikamwamini.


Hatimaye tukaifikia nyumba ya wageni aliyoikusudia. Nje ya nyumba hiyo kwenye uchochoro mmoja kulikuwa na watu wanaokunywa pombe, wake kwa waume. Mwenyeji wangu alionekana mwenyeji hapa. Alimwita mmoja wa watumishi wa nyumba hiyo kwa jina, “Rehema! Mpe chumba mjomba wangu. Mchagulie chumba safi. Sawa?”


Rehema, msichana mkubwa mnene, aliyeonekana kalewa aliniashiria kumfuata. Nyumba haikuwa na umeme. Mishumaa miwili, mmoja uliowekwa mlango wa mbele na mwingine mlango wa nyuma ndiyo iliyotuongoza. Niligeuka








ili kumshukuru mwenyeji wangu. Hakuwepo. Alikwishapenya uchochoro mwingine na kuondoka zake. Nikamfuata Rehema. “Unataka chumba che bei gani?” Aliniuliza. “Vipo vya


elfu mbili na elfu na mia tano.” “Nipe cha elfu na mia tano.”


Kilikuwa chumba cha uwani, kidogo sana. Dirisha lilikuwa moja, dogo vilevile. Kitanda chao kilitosha mtu mmoja tu, si zaidi.


“Kinakufaa?”


“Kinafaa sana.” Nilimjibu.


“Ngoja nilete mshumaa. Umeme umekatwa huu mwezi wa tatu. Na kishoka leo kachelewa kuja.”


“Kishoka ndiyo nani?” nikaomba kuelewa.


“Jamaa yetu ambaye huja usiku kuturudishia umeme. Asubuhi sana huja tena kuukata kabla TANESCO hawajapita mitaa hii,” alifafanua.


“Kwani mnadaiwa pesa nyingi?” nilihoji.


“Nyingi sana. Kama milioni tatu na laki sita hivi. Maji yenyewe mwaka wa nne hayajatoka. Lakini bili yao imefika laki tisa na nusu.”


Nikashangaa. Kwa hesabu za haraka haraka nyumba hiyo, yenye vyumba sita pekee na baa ya uchochoroni haikuwa na uwezekano wa kupata walao laki mbili kwa mwezi. Gharama hiyo ya umeme na maji ilitokea wapi? “Mtalipa?” nilimuuliza.


“Nani alipe? Unalipa deni linalolipika. Lisilolipika unaachana nalo,” alinisomesha.


Rehema alipoondoka nilipanda kitandani kwangu kulala. Ndio kwanza nikabaini kuwa godoro lilikuwa kuukuu, pengine halikupata kubadilishwa toka nyumba hiyo ilipojengwa. Mbavu zangu zilikwenda moja kwa moja kukutana na chaga








za mbao. Si hilo tu, dakika mbili tu za kupumzika juu ya kitanda hicho, nilikaribishwa na mbu na kunguni. Wakati mbu wakiuma baada ya kelele zao za vitisho masikioni, kunguni wao walinitesa kwa kufyonza damu yangu kimyakimya na kunisababishia maumivu mengine. Nilifanikiwa kuwaua kunguni wawili watatu. Lakini harufu yao kali na damu nyingi toka kwa wateja wao ilinitia kichefuchefu


Adha ya tatu ilikua ikinisubiri. Joto. Chumba kilichemka kwa joto kama tanuru. Nikainuka na kufungua lile dirisha pekee. Tendo hilo lilileta karaha badala ya faraja. Harufu nzito, ya kutisha iliyoingia chumbani humo toka dirishani ilinifanya niamke na kumwita Rehema. “Harufu hii ya nini?” nilimuuliza. “Hilo dirisha huwa alifunguliwi!” alinionya akilifunga


mara moja. “Kuna mfereji wa maji machafu hapo. Haujazibuliwa leo mwaka wa sita. Kwa hiyo, maji yametuwama uchafu umeoza na kufanya harufu ya kutisha.”


“Kwa nini hauzibuliwi?” “Sijui”


Nikazidi kushangaa. Mambo gani haya ninayoyashuhudia, siku moja tu baada ya kutoka jela. Kama maisha ya uraiani ndiyo haya, malazi ndiyo haya, iko wapi tofauti ya kuishi uraiani na gerezani?


Tofauti kati ya maeneo ya Manzese na katika ya mji pia ilinishangaza sana. Wakati kule kulionekana kama Peponi huku hakukutofautiana sana na Jehanamu. Kama ungetokea moto, uteketeze nyumba moja ni dhahiri kuwa mamia ya nyumba yangeungua na maelfu ya watu kupoteza maisha. Nikaelewa kwa nini yanapozuka maradhi kama kipindupindu na hata UKIMWI hayaondoki kabla ya kuteketeza mamia ya watu katika maeneo kama haya. Huu ndio uhuru tulioupigania na kuupata? Nilijiuliza. Huu ndio Ujamaa niliousikia mara








kwa mara toka gerezani? Au ndio Azimio la Arusha lililopigiwa sana kelele?


Wakati nikiwaza hayo jambo la ajabu likatokea. Umeme uliwaka. Kishoka alikuwa amefika nadhani. Feni chafu lililokuwa darini likapata uhai. Ama liliwafukuza mbu ama waliogopa kelele zake, kwani niliona mbu wakipungua ghafla. Kunguni nao walijificha. Nikapanda kitandani na kujilaza. Usingizi ukanichukua.


Niliamka kesho yake saa tatu. Nilikuwa mgeni peke yangu katika nyumba hiyo. Rehema alikuwa akipita chumba hadi chumba kukusanya shuka kwa ajili ya kuzifua. Alinionyesha bafu ambalo lilikuwa na maji ya ndoo, kipande cha sabuni ya mchi kikiwa pembeni. Nilioga na kujisikia nikiburudika kidogo, hali ambayo ilinifanya nisikie njaa ikianza kulitekenya tena tumbo langu. Niliishtakia kwa Rehema ambaye alinielekeza uchochoro wenye ‘mama ntilie’ pekee eneo hilo. Nilimpata. Nikanywa chai ya shilingi hamsini, chapati mbili za mia na maharage ya mia. Chakula na bei vilinifuraisha sana.


Nikaanza kazi ya kutafuta njia ya kurudi barabarani. Nilielekezwa mara nne na kupotea mara mbili kabla ya kumwuliza bwana mmoja mtanashati ambaye aliniambia nimfuate.


“Ni afadhali kupotea New York, kuliko katika vichochoro vya Manzese. Humu unahitaji akili za ziada kujua njia ya kwenda na kutoka kwako,” alisema kiongozi wangu huyo mpya wa msafara.


“Kwa nini inakuwa hivi?” Nilimuuliza. “Umeshafika mwanza?” Alinijibu kwa swali jingine. “Zamani sana.”


“Fika sasa hivi uone,” alisema “Kule watu wanajenga hata juu ya mawe. Ile mandhari nzuri ya asili imepotea kabisa








kwa ajili ya watu kutafuta makazi ya kuishi. Tatizo unaloliona hapa



Jane aliweza kumfuatilia sokwe toka anazaliwa, anakua, anabalehe hadi naye anapata mtoto, alinukuu mwenendo na tabia zao, chakula chao, tiba zao na hulka zao mmoja baada ya mwingine. Alimfahamu kila sokwe na kila familia ya sokwe vilivyo, kiasi cha kujua nani kiongozi wao, nani anapinduliwa uongozi na nani kapindua. Utafiti makini wa aina yake duniani ambao tayari umempatia shahada ya udaktari.


“Unajua hujaniambia jina lako?” Alinizindua. “Naitwa Petro Mtukwao Kionambali,” nilimjibu.


Jane alifahamu Kiswahili kidogo sana. Kati ya machache aliyoyafahamu jina la ‘Mtukwao’ au ‘Kionambali’ lilimpa maana fulani, lakini hakuweza kuifafanua mara moja. Aliyataja majina hayo mara mbili tatu, akikosea, kabla hajakata tamaa na kuniuliza maana yake, “Petro bila shaka ni Peter kwa Kiingereza. Ni jina lenye asili ya Kigiriki likiwa na maana ya mwamba au jabali. Hii Kionambali au Mtukwao ina maana gani?”


Jane alinitazama , “Ni la Kiebrania,” nilimjibu. “Lina maana ya Mungu ni mwenye fadhila sio?” nilimuuliza kabla ya kumjibu.


Jane alionyesha mshangao. Nadhani hakutegemea kuwa pamoja na hali niliyokuwa nayo ningeweza kufahamu mambo mengi kama ilivyokuwa. “Ni kweli kabisa,” alijibu baada ya tabasamu fupi, “Kiona mbali?” alisisitiza.


Wazazi wangu hawakupata kuniambia maana hasa ya majina yangu. Nadhani yalitolewa na babu kwa sababu zake.








Hata hivyo nilimweleza Jane hili na lile juu ya maana ya majina hayo.


Sidhani kama aliridhika. Mara nilimwona akibadilika ghafla kama mtu aliyekumbuka jambo “Kionambali…. Mtu kwao… nadhani nilipata kuyasikia majina hayo kabla ya leo,” alisema.


Nikacheka. “Unacheka nini?”


“Nina hakika hujawahi kulisikia mahala popote. Ni jina dogo sana katika nchi hii. Sijawahi kuandika kitabu wala kucheza mpira hata nijulikane.”


“Hapana, nimelisikia likitajwa. Si mara moja si mara mbili,” alisisitiza.


Sikuamini. Nikijua kuwa alitokea kwao Uingereza, akakaa Kenya kwa muda kabla ya kuja nchini sikuona vipi angeweza kukutana na jina langu. Hasa ikizingatiwa kuwa muda mwingi nilikuwa gerezani.


“Unakwenda wapi?” alinihoji. “Kigoma.”


“Nyumbani kwenu?” “Ndiyo.”


“Kwa hiyo, safari yetu moja.” “Bila shaka.”


Alisita kwa muda kabla hajauliza swali jingine, “Kwa hiyo, unakwenda likizo?”


“Ndiyo na hapana,” nilimjibu. “Una maana gani?”


“Nina maana kuwa ndiyo nakwenda nyumbani; hapana siendi likizo.”

Jibu langu lilimshangaza Jane, “Kwani unatokea wapi?”


Sikuona sababu ya kumficha, “Jela.”


Kiasi nilimwona akishtuka. Lakini, akiwa mwanamke mwenye roho ya chuma, anayeweza kuishi na kuvumilia hasira za ghafla za wanyama hatari kama sokwe, alijirekebisha mara moja. Badala yake aliniuliza kwa upole, “Nini kilitokea?”


Alikuwa binadamu wa kwanza uraiani aliyetaka kujua masaibu yangu toka nilivyofungwa hadi kufunguliwa. Akawa binadamu wa kwanza niliyepata kumsimulia, kwa tuo, yote yaliyonitokea hadi nikatupwa gerezani kwa miaka mingi. Sijui kwa nini niliamua kuwa wazi kwake. Nadhani ni kwa kuwa sikuwa na shaka kuwa ni mtu mwenye huruma sana. Kama anaweza kuishi na sokwe…


Nilipofika sehemu ambayo nilimtaja Dakta Leakey kama mwajiri wangu pekee ambaye niliishi naye kwa muda mrefu nilimuona Jane akishtuka. Mara akanikatiza kwa kuuliza, “Leakey yupi?”


“Leakey unaemjua wewe. Na mke wake Mary… wagunduzi wa fuvu la kale zaidi nchini,” nilimjibu.


Jane aliinuka na kunikodolea macho ya mshangao. “Sasa nimefahamu wapi nilisikia jina lako kwa mara ya kwanza,” alisema baadaye.


“Wapi?”


“Kwa akina Leakey. Walikuwa hawaachi kukutaja. Walishangazwa sana na kutoweka kwako ghafla, bila kuaga, mtu ambaye walidai kuwa walimtegemea sana katika shughuli zao.”


Ikawa zamu yangu kushangaa, “Unawafahamu?” “Vizuri sana,” Jane alinijibu. “Walipata kuniajiri pia.


Kutokana na mapenzi yangu kwa wanyama na mazingira








Leakey alinishawishi kwenda kwenu Kigoma kufanya utafiti


wa wanyama wale, binamu zetu.”


Sikuwa na la kusema, nikauliza, “Hawajambo?” “Nani?”


“Akina Leakey.”


Jane akacheka, “Wazima sana. Kwa nini ulifanya vile?” “Kufanya nini?”


“Kufungwa.Kukubalikufungwabilakuwaarifu.


Wangeweza kukusaidia.”


Ilikuwa wazi kuwa Jane hajui maana ya kufungwa, hasa katika nchi zetu za dunia ya tatu. Mnyama anayefugwa ana uhuru mara mia zaidi ya mfungwa.


Wakati nikizungumza na Jane nilimwona msichana mmoja, msafiri kama sisi, akinitazama sana. Nilimtupia macho. Nikamwona akiyakwepa macho yangu kwa namna ya haya kiasi. Kitu fulani kilinifanya nipate hisia kuwa namfahamu. Wazo ambalo nililipuuza mara moja. Jana tu nimetoka jela, nitamjulia wapi msichana huyu?


Kitu kimoja kilinivutia kumtazama msichana huyu alikuwa ana tofauti kubwa na wasichana wengine wengi niliowaona jijini hapo. Alikuwa Mwafrika halisi. Nywele zake zilikuwa fupi, ambazo hazikupata kuathiriwa na madawa. Ngozi yake laini maji ya kunde, pia haikuwa na dalili zozote za kuathiriwa na madawa hayo. Hata mavazi yake yalikuwa ya heshima. Gauni jekundu lililomkaa vizuri lilimfunika hadi miguuni.

Lakini kuna kitu cha ziada ambacho kilinivutia zaidi kwa msichana huyu. Halikuwa umbile lake wala mavazi yake. Kilikuwa kitu fulani. Kwa bahati mbaya sikuweza kubaini mara moja ni kipi hasa kilichonivutia zaidi kwake. Ningeweza








kukisomakituhichokatikamachoyake,lakinitayari aliyakwepa macho yangu na kutazama upande mwingine.


Honi ya treni iliyokuwa ikiingia stesheni iliniokoa kujibu swali la Jane pamoja na kuendelea kusumbua fikra zangu juu ya msichana yule. pilikapilka za kuingia katika mabehewa zikaanza. Mimi nikiwa sina mzigo wowote nilifanya kazi ya kumsaidia kupakia vitu vyake katika chumba cha daraja la pili alicholipia. Mimi, nikiwa sina namba ya kiti, nilipata debe moja la msafiri mwenzangu na kulikalia. Roho yangu ilipumua pale dakika ishirini baadaye treni ilipoanza safari ya kuelekea bara.


Jing... jang… jing… jang… tuliuacha mji na kuingia Buguruni. Jing… jang… jing… jang … vingunguti. Jing… jang… jing… jang… Karokota. Taratibu tukauacha mkoa wa Dar es Salaam na kuingia Pwani. Tulizipita stesheni za Soga, Ruvu na Magindu kabla hatujaiacha Pwani na kuingia Morogoro katika stesheni za Kidugalilo, Ngerengere, Mikesa na hatimaye Morogoro mjini.


Wakati huo usiku ulikwishaingia. Sikuweza kuziona vizuri stesheni za Mkata, Kimamba na ile ya Kilosa. Toka hapo tuliingia stesheni ya mpaka wa Morogoro na Dodoma, Kidete kabla ya kufika Godegode, Gulwe na Kikombo. Tulifika Dodoma alfajiri ya siku ya pili.




Jane alikuwa akinitafuta. Alinikuta nikiwa nimeegemea mlango nikijaribu kupata chochote ambacho ningeweza kupata juu ya mji wa Dodoma, makao makuu ya serikali baada ya kuhamishwa toka Dar es Salaam. Zaidi ya majengo kadhaa, barabara pana zaidi na watu wa kutosha zaidi bado Dar es Salaam niliyoiacha jana ilifanya Dodoma ionekane kama mzaha kuiita makao makuu.








“Unajisikiaje?” Jane aliniuliza


“Safi kama chuma cha pua,” nilimjibu


Akacheka. “Twende tukapate kifungua kinywa,” aliniambia.


“Wapi?”


“Mgahawa wa humu ndani.”


Nikamfuata. Tulipita mabehewa kadhaa kabla ya kufikia behewa la chakula. Tukaketi. Aliagiza chapati mbili, supu ya kuku na chai kwa kila mmoja wetu. Kwangu ulikuwa mlo ambao sitapata kuusahau kwa muda mrefu. Toka nilipopata chai na maharage ya ‘mama ntilie’ kula Manzese tumbo langu lilikuwa halijaonja chakula zaidi ya karanga za mia moja nilizonunua humo ndani.





Tulikula taratibu. Kila mara Jane akinidodosa juu ya mipango niliyokuwa nayo baada ya kutoka gerezani. Hakunielewa pale nilipomwambia kuwa nilikuwa na mpango mmoja tu katika akili yangu, ambao haukuwa ziadi ya kufika nyumbani, kumwona babu na wazazi wangu, kama wako hai.” “Bila shaka ulitoka kwenu mikono mitupu… unataka


kurudi mikono mitupu?” alinihoji. “Sina jinsi.”


“Kwa nini?”


Asingeweza kuelewa. Asingeelewa hata kidogo hata kama ningemwelewesha vipi. Kwamba lazima nikaombe radhi kwa kupoteza hirizi! Kwamba nina hakika mikosi na balaa nyingi ninazopata zilitokana na kuipoteza baraka ile, hivyo lazima nioshwe kwa kutemewa mate usoni. Mzungu, mwenye utamaduni tofauti na wangu angeelewaje? Sikujisumbua kumwelewesha.








Jane akaamua kuifichua siri iliyokuwa moyoni mwake. Alinitaka twende wote Gombe nimsaidie kazi. Kwamba alikuwa na mipango ya kufungua kituo kingine cha sokwe kusini mwa ziwa Tanganyika, katika milima ya Mihale, kilometa zipatazo


120 toka mjini Kigoma. Kwa mujibu wa Jane milima hiyo ilikuwa na sokwe waliokadiriwa kuwa 700 katika makundi kama kumi na mitano. “Siwezi kufanikisha peke yangu. Lazima niwe na mtu mwaminifu, mwadilifu na pia tunayeelewana lugha vizuri,” alisema


“Halafu,” aliongeza. “Mume wangu ana mpango wa kutengeneza filamu kubwa, itakayojumuisha vivutio mbalimbali vya Tanzania. Kwa historia yako na uzoefu wako hakuna mtu ambaye atamfaa zaidi yako.”


Hili la pili lilinivutia zaidi. Ningependa sana kuwa sehemu ya historia ya mtu atakayefanikisha kazi hiyo. Lakini nilikwishajiwekea nadhiri ya kutojihusisha na jambo lolote kabla ya kufika kwetu. Ama niwaone wazazi wangu, ama niyaone makaburi yao.


Nilimweleza hivyo Jane. Bado hakunielewa. Lakini hilo lilikuwa tatizo lake, halikuwa langu.


Safari ya mchana ilivutia zaidi. Tulisimama dirishani mimi na Jane tukiangalia nje, kituo baada ya kituo. Nkungu, Nala, Bahi, Kintinku, Saranda, hatimaye tukaingia Manyoni. Watu na mazingira maeneo yote haya havikunifurahisaha sana. Ardhi ilijaa vumbi, mtu mmoja hapa na pale. Hali iliyonifanya hisia za nusu jangwa zinijie akilini. Hali kadhalika hali za wakazi wengi iliashiria umasikini mkubwa. Mavazi ambayo wengi wao walivaa, baadhi wakitembea bila hata kandambili. Ilikuwa dalili tosha ya umasikini. Hata wale waliokuwa na bidhaa, bidhaa zao ziliashiria kuganga njaa tu. Mtu mzima








akiwa na vichane vitatu vya ndizi, mwingine akiwa na chupa moja ya asali, yule sinia la karanga! Kwa gari moshi ambalo hupita hapo mara mbili tatu kwa wiki sikuona kama biashara hizo zilikuwa na namna yoyote ya kuwaondoa katika vibanda vya tembe tulivyokuwa tukiviona toka tunaingia Dodoma hadi tunaiacha.


Stesheni ya Manyoni ilishamiri kwa biashara ya kuku, walio hai kwa waliokaangwa.

Takribani kila mtu alikuwa na sinia yenye mapaja ya vidari vya kuku wanaotamanisha kuwala. Bila shibe ya mlo alionipa Jane ningejikongoja kununua paja moja. Ingawa baadhi ya watu hudai kuwa hawa si kuku wa kawaida kwa ajili ya wingi wao. Wanadai baadhi ya tunaowadhania kuku waliokaangwa ni kunguru na ndege wengine wa porini waliozagaa katika maeneo hayo. Kwa kweli, ulikuwa mzaha wa watani wa Wanyaturu na Wanyiramba.


Toka Manyoni tuliingia Itigi, kaskazini hadi Malingwe. Jua likaanza kuzama. Jane alirudi chumbani kwake kujisomea kitabu mimi nikaendelea kuranda ndani ya mabehewa hayo mengi. Tukafika Nyama, tukaingia Igagula. Saa mbili za usiku tulifika Tabora. Hapo tulichukua muda mrefu kutokana na pilikapilika nyingi za kubadili mabehewa, kukagua vichwa vya treni na pengine kufanya ukarabati.


Nilitamani kuutumia muda huo kuchepuka kidogo nikautupie macho, walao kidogo mji wa Tabora, ambao uko kidogo nje ya stesheni hiyo. Hata hivyo kwa kuchelea kuachwa sikuthubutu. Niliishia kuchungulia tu nje ya stesheni ambako niliiona ile miembe iliyozeeka lakini bado ilikuwa ikipamba na kuzaa embe tamu za dodo na bolibo.


Niliona pia kundi kubwa la mbuzi wasio na mlinzi wakirandaranda kando ya barabara hiyo. Mbuzi wa Tabora?








Nilijiuliza nilipokumbuka simulizi ya mji wa Tabora kuwepo na mbuzi wengi wasio na mmiliki ambao hutembea ovyo mitaani bila kubugudhiwa, mbuzi ambao inaaminika kuwa kwa namna moja au nyingine wanahusiana na ama ushirikina ama laana fulani. Mwenyewe alifariki zamani na kufanya wawe hawana mwenyewe, lakini kila mtu ambaye huthubutu kuwala hudhurika na hata kupoteza maisha. Jambo ambalo lilisababisha hata wezi wa mjini hapo wawaogope.


Honiyakuashiriasafariikapigwa.Nikarudiau kuparamia behewa lolote lililokuwa karibu. Dakika tano baadaye safari ikaanza. Ilikuwa awamu ya mwisho ya safari hiyo ndefu ya kilometa 2600 toka Dar es Salaam hadi Kigoma. Hamu niliyokuwa nayo ya kufika nyumbani ikaanza kuingia nyongo. Hofu ikaanza kuchukua nafasi. Hofu ya kutojua lipi nitalikuta huko nyumbani. Habari za kufurahisha au kuhuzunisha, heri au shari. Hali kadhalika, aibu ya kurudi mikono mitupu kama nilivyoondoka, baada ya miaka nenda rudi ya kuhangaika pia ilinitesa sana. Sio siri, nilitamani garimoshi hilo lipate ajali, mtu mmoja tu apoteze maisha;


Petro


Haikuwa. Treni iliendelea kukata mbuga. Ikiwa safari ya usiku sikuweza kuona mabadiliko ya ardhi toka ile ya nusu ukame. Ya Dodoma hadi Tabora hadi ile yenye rutuba nyingi ya kutokea Tabora hadi Kigoma. Kelele za wasafiri kila tulipofika stesheni ndizo ziliniashiria tuko wapi; Usoke, Kaliua, Suinge, Malagalasi, Uvinza, Simbo, Luiche na hatimaye Kigoma


Ulikuwa mkesha wa aina yake. Pilikapilika za kuingia katika mabehewa kila stesheni zilikuwa kubwa na za fujo kubwa. Mizigo ilirushwa ndani ikifuatiwa na wababe; wake kwa waume. Ilikuwa rahisi kwa mgeni kufikiria kuwa watu










wa Kigoma wana asili ya vurugu. Lakini kamwe mwenyeji asingeweza kufikiria hivyo. Watu hawa hawakuwa na njia nyingine yoyote ile ya usafiri. Maeneo mengi hayakuwa na barabara iliyowaunganisha na upande mwingine wa dunia zaidi ya treni. Hivyo, kuachwa na usafiri huo kulimaanisha kuharibikiwa kwa mipango yako ya safari pengine kwa wiki nzima au zaidi. Hivyo, kutumia nguvu na ubabe lilikuwa jambo la lazima.


Tulifika Kigoma saa moja na nusu za asubuhi, lakini kwa sababu za kijiografia ndio kwanza jua lilikuwa likichomoza. Miale yake ilipenya milima ya Bangwe na kutuangazia pale stesheni, kando kabisa mwa Pwani ziwa Tanganyika. Ziwa ambalo liliupokea mwanga huo, likaujumuisha na maji yake yasiyo na rangi na kufanya limeremete kwa mchanganyiko wa nuru ya rangi ya dhahabu toka angani na buluu toka katika lindi la maji na kutoa sura ya kusisimua sana.


Nilishuka na kusimama kwa muda hapo nje nikitazama huku na kule kana kwamba siamini kuwa nimerejea nyumbani. Macho yangu yalivutwa na jengo imara la stesheni hiyo, lililojengwa na Mjerumani toka enzi zile. Zaidi ya ukarabati wa rangi na pengine bati jengo lile lilikuwa imara kama walivyoliacha. Wala halikuwa na dalili zozote za kupoteza uimara wake katika siku za usoni.


Nikahamisha macho kwenye jengo na kuyatupa ziwani. Kwa mbali, niliweza kuona mitumbwi na mashua za wavuvi wakirejea Pwani baada ya shughuli zao za usiku kucha, lakini kilichovutia zaidi macho yangu ni meli kubwa, yenye rangi nyeupe iliyotia nanga katika bandari hiyo. Jina lake liliweza kusomeka hapo niliposimama, MV LIEMBA.


Hii ni mali yenye historia ya pekee duniani. Kwanza,

inaaminika kuwa ni meli ya kale kuliko zote duniani ambayo bado inafanya kazi. Pili, imezitumikia enzi zote muhimu za historia ya Tanganyika ikiwa imeletwa na kuunganishwa na Wajerumani miaka ya 1914 na kupewa jina la Graf Von Goetzen. Mjerumani alipozidiwa katika vita ya pili aliizamisha katika lindi la ziwa Tanganyika wa nia ya kumkomoa Mwingereza aliyechukua madaraka. Lakini wao walifanya kila jitihada kuiibua majini na kuitengeneza. Ikaanza kazi kwa jina jipya la SS Liemba. Tanganyika ilipopata uhuru wake Liemba ilikarabatiwa tena na mitambo yake badala ya kutumia mvuke ikawa ikitumia dizeli, hivyo ikaitwa MV Liemba. Meli hiyo hadi sasa ni tegemeo kuu la usafiri katika mwambao wa ziwa Tanganyika hadi bandari za Mpulungu Zambia, Bunjumbura, Burundi na Kelemie Kongo.


Upande wa pili wa ziwa hilo macho yangu yalivutwa na baadhi ya milima ya nchi hizo. Burundi kwa upande wa kaskazini na Kongo ilionekana mbele yangu, magharibi ya nchi yetu. Hali ya hewa ikiwa safi, anga likiwa angavu niliweza kuiona milima ya nchi hizo kwa uwazi kabisa.




Sijui ningesimama hapo kwa muda gani kama nisingeshikwa bega na nilipogeuka nikakutana na uso mpole wa yule msichana aliyenivutia pale stesheni ya Dar es Salaam. Sura yake ilikuwa iliyojaa haya. Hata hivyo, alijitahidi na kuniuliza kwa sauti yake ya upole, “Samahani kaka. Hivi unaitwa Petro Kionambali?”


“Naam,” nilimjibu.


“Ulipata kuishi katika maeneo ya Bonde la Ufa?” aliongeza swali jingine ambalo pia nililikubali. Nikamwona akibadilika sura. Kwanza alitabasamu. Kisha tabasamu lake likamezwa na uso uliojaa huzuni, machozi yakimlengalenga machoni.








“Vipi kwani?” nilimwuliza kwa mshangao. “Petro… Hunikumbuki?”


Sikuweza kuelewa anachozungumza. “Nakumbuka kukuona juzi pale stesheni, Dar es Salaam, kwa mara ya pili nakuona leo hapa Kigoma,” nilimjibu


Pamoja na machozi yake nilimwona akitabasamu kisha alisema, “Petro wewe ulipata kuokoa maisha yangu kwa kuhatarisha yako. Ulinichukua hadi Singida ambako ulinipeleka misheni ambako walinilea kiimani na kielimu. Sasa hivi nina kazi nzuri hapa Kigoma.”


Akili zangu zilikimbia na kunirejesha nyuma zaidi ya miaka ishirini iliyopita. Nikamwona yule msichana wa Kimasai aliyekuja katika kambi yangu huku akitetemeka. ‘...Nisaidie


...Naogopa’ Nilikumbuka jina lake, “Nashifa sio?”


Nilimwona akichangamka. “Unalikumbuka hata jina langu? Hata hivyo nilibatizwa na kupewa jina jipya la Maria. Lakini sijaliacha jina langu la asili. Nimefurahi sana kukuona Petro. Siku zote nilikufikiria usiku na mchana. Nilikuwa na hakika kuwa ingetokea siku nikakutia machoni. Imetokea…” alisita kuzungumza na kuangua kilio.

eb 4, 2021

Thread starter

Add bookmark

#193

Sikujua kilichotokea nilijikuta nimemkumbatia kwa namna ya kumfariji huku yeye pia akinikumbatia na kukilaza kichwa chake juu ya kifua changu akiendelea kulia huku akinong’ona maneno fulani ambayo sikuyasikia vizuri. Nilisikia machache tu, “Uliokoa maisha yangu… kwa gharama ya kuharibu yako… sikupata kujisamehe kwa kitendo kile…”


Nilicheka kidogo kabla ya kumnong’oneza vilevile, “Maisha yangu ni hadithi nyingine. Masaibu yako hayahusiani hata kidogo na yale yaliyotokea. Yangu nayajua mimi na Mungu wangu.”








Tulikuwa bado tumekumbatiana. Kama si macho ya wapita njia kututazama kwa mshangao sijui tungekaa katika hali hiyo kwa muda gani. Macho yao yalifanya nijikumbuke na kujitazama. Nilitoa picha ya kuchekesha sana kwa mavazi yangu ambayo hayakuwa zaidi ya midabwada, kumkumbatia msichana huyu mtanashati ambaye sasa alivaa vitenge vilivyomkaa kana kwamba alizaliwa navyo. Nikajikwanyua toka mikononi mwake na kumtaka radhi.


“Samahani ya nini? Huju nilivyofarijika Petro.” Alisema. “Lakini tayari njia zetu zimetofautiana sana. Mimi ni ndege wa jela asiyestahili kukukumbatia hadharani. Tazama


nilivyo,” nilisema nikijitenga naye zaidi ili anione vizuri zaidi.


Kwa mshangao wangu alicheka kabla ya kusema, “Najua yaliyokusibu. Nilikuwa nikifuatilia kwa karibu maongezi yako na yule mama wa Kiingereza. Anaitwa nani vile, Jane siyo?”


Nilikubali kwa kichwa.


“Hivyo huna haja ya kuniambia chochote zaidi. Najua umerudi kwenu. Najua umerudi mikono mitupu. Usijali. Nitakusaidia kadri ya uwezo wangu. Uliniokoa kwenye mvua mimi pia nitakuokoa kwenye jua.”


Alitia mkono wake kwenye pochi lake la mkononi na kutoa kadi ambayo alinikabidhi. Ilikuwa na majina yake na namba za simu. Kilichonivutia zaidi ni cheo chake. Afisa uhamiaji wa mkoa! Niliduwaa.


“Matunda ya wema wako hayo.” Alinifafanulia. “Wamisheni wale walinipa elimu bora hadi chuo kikuu.


Mara kadhaa nimepelekwa nje kuongeza ujuzi. Huu ni mkoa wangu wa tatu toka nilipopanda cheo.”


Nilizidi kuduwaa. Safari hii aliniondoa mshangao kwa kunishangaza zaidi. Alitia tena mkono wake mfukoni na








kunipa kitita cha fedha. Kwa hesabu za haraka haraka zilipata kuwa shilingi laki moja.


“Za nini?” nilimuuliza.


“Zitakusaidia kidogo. Najua una matatizo mengi. Fika


nyumbani, wasalimu wazazi halafu njoo mjini tushauriane.”


Nilitamani kulia. Kwa nini siku zote maisha yangu yamekuwa ya kukutana na binadamu wenye roho mbaya kama shetani na wale wenye roho nzuri mfano wa malaika? Nilijiuliza huku nikiwa nimemkodolea macho. Unajua wewe ni malaika. Unajua utafika mbinguni? Nilitamani kumwabia hivyo. Nilishindwa. Badala yake nilijikongoja kumwuliza, “Umeshaolewa?”


Alinipa jibu jingine ambalo liliniacha taabani zaidi, “Nilikuwa nikikusubiri wewe.” Nilipomtazama, aliyaepuka macho yangu na kutazama chini. Mara nikaelewa kilichonivutia zaidi juu yake. Haya! Pamoja na elimu yake, pamoja na cheo chake, bado alikuwa msichana wa kiafrika halisi, mwenye uso wa soni tofauti kabisa na wasichana wengi wa kileo.


“Sina budi kuondoka,” aliseme. “Tafadhali tuwasiliane.


Sawa Petro Kionambali?” “Bila shaka.” Nilimjibu


Akaifuata gari ambayo muda wote ilisimama nje ya stesheni ikimsubiri. Akaingia upande wa pili wa dereva na kupunga mkono wakati gari ikitiwa moto na kuondoka.


Mara alipotoweka machoni mwangu, nilihisi upweke wa pekee ambao sikupata kuujua huko nyuma.


Nilizihesabu tena fedha alizonipa. Nilikuwa na laki moja na hamsini. Sikuhitaji kufikiria sana. Niliendea duka la karibu la nguo na kununua shati mbili, suruali mbili na shuka la kujifunika.








Nilikuwa na mfuko wa nguo mpya mkononi ndiyo kwanza nilijiona nilivyochakaa. Nilikuwa nanuka!. Niliweza hata kuisikia harufu chafu ya mwili wangu mimi mwenyewe. Jasho la joto la Dar es Salaam na vumbi la Dodoma, purukushani za Tabora na malazi mabaya ndani ya behewa lililotoa mchanganyiko wa kutisha. Nikaamua kuiacha bandari na kuufuata ufukwe nikielekea Mtanga hadi nilipopata sehemu faragha ambayo nilivua nguo zangu na kujitupa ziwani. Sikuwa na sabuni wala mswaki. Nilitumia mchanga na vidole kujisugua. Nikapiga mbizi mara mbili tatu. Kweli, aliyeogelea hafi maji, kwani nilijikuta nikielea juu ya maji kana kwamba maisha yangu yote nilikuwa ziwani humo.


Nilipotoka majini nilijihisi mtu mpya. Hisia fulani ziliniambia kuwa kwa kuoga katika ziwa hili lenye historia ya pekee nilikuwa nikisafisha mikosi na mikasa yote iliyoniandama na kuanza maisha mapya.


Pengine haikuwa uongo. Ziwa Tanganyika lilikuwa mwujiza mwingine wa dunia. Kwanza lilikuwa refu kuliko maziwa yote duniani. Pia, kina chake kwenda chini kilivunja rekodi ya maziwa yote ya ulimwengu.


Likiwa limeenda chini kwa takribani meta 2400 toka kilele cha milima ya Mahele iliyopo kilometa 150 toka Kigoma mjini au meta 1500 toka ardhi ya kawaida ya mkoani humo mwisho wa kina hicho uliwiana na usawa wa bahari kwa miji ya Dar es Salaam na Zanzibar. Inaaminika kuwa kuwepo kwa ziwa hilo ni matokeo ya mabadiliko makubwa yaliyopata kuitokea dunia, kama matetemeko ya ardhi au volkano ambayo pia yanaaminika kuibua vitu kama Bonde la Ufa. Walikotokea samaki ainaaina na viumbe wengine hai waliomo tele ziwani humo ni fumbo jingine ambalo mwanadamu hajapata kulipatia ufumbuzi.








Sikuhitaji gari kutoka kigoma hadi Mwanga. Mwendo wa dakika ishirini kwa mguu uliniwezesha kufika katikati ya mji huo. Mwanga ilichangamka. Vijana waliokuwa wakifanya kazi za kushevu walikuwa tele katika ofisi zao zinazovutia kwa vioo na viyoyozi. Niliingia katika kimojawapo cha vibanda hivyo na kukinga kichwa changu.


“Nywele na ndevu,” nilisema.


“Utahitaji tukuwekee na super black, kaka?” niliulizwa na kijana huyo


“Kwa nini?”


“Mvi zinakuanza. Unaona hapa?” alielekeza.


Nikajitazama katika kioo. Kweli, kulikuwa na mvi mbili tatu katikati ya kichwa changu. Nazeeka! niliwaza kwa mshtuko kidogo. Kuzeeka kabla ya kufanya jambo lolote ambalo familia, jamii na nchi yangu itaweza kujivunia haikuwa dhamira yangu hata kidogo.


“Hapana, shevu tu,” nilimwambia. Sikuona haja ya


kuficha shahada ya umri wangu.


“Ndevu unashevu kwa mashine au magic?” “Ndiyo nini hiyo mejiki?”


Akanionyesha dawa fulani. “Hii inafanya kidevu kiwe kama cha mtoto mdogo,” Alifafanua.


“Na bei yake?” “Iko juu kidogo.”


“Kama ni hivyo tumia mashine.”


Muda mfupi baadaye nilikuwa mtu mwingine kabisa, mtu anayependeza kwa usafi hasa kwa kijana huyo kunipaka mafuta ambayo yalilainisha ngozi yangu. Nilijitazama kwenye vioo vyake, mbele na nyuma, kwa muda kabla ya kumlipa na kuondoka.








Niliuliza magari ya kwenda Kasulu. Niliambiwa kuwa nimekwishachelewa, kwamba lilikuwepo basi moja tu la Mwarabu ambalo huondoka saa kumi na mbili za asubuhi kila siku.



Pia, nilidokezwa kuwepo kwa malori ya mizigo ambayo huondoka asubuhi hadi saa tatu. Nilipoitazama saa yangu iliitimu saa nne na nusu za asubuhi. Nikaamua kutafuta hoteli ya bei nafuu ili nijipumzishe hadi hiyo kesho.


Kabla ya kuchukua chumba niliamua kuuvinjari kidogo mji wa Mwanga. Kama miji mingine nchini Mwanga ilipanuka sana. Maeneo kama Vumilia na Majengo ambayo zamani yaliogopwa na kudharaulika sasa viwanja vyake vilioneka lulu. Majengo yalikuwa yakiota kama uyoga. Kwa bahati mbaya sana, kama yalivyokuwa maeneo mengi mapya, maeneo haya pia yalikosa huduma muhimu. Hayakuwa na mifereji ya maji machafu, hayakuwa na mfumo wa maji safi, umeme wa barabarani ilikuwa ndoto na hata barabara zilijaa na kujitunza zenyewe. Hali iliyopelekea mafuriko na uchafu kuivuruga dhamira nzima ya wamiliki.


Nilienda Mwanga Katubuka. Nikaingia Sokono. Macho yangu yalikuwa yakiwatafuta samaki niliowazoea na wale ambao nimekuwa nikisikia sifa zao toka utotoni; nonzi, wale samaki wakubwa wanaofanana na ndege, kuhe, samaki mtamu ambaye ana hadhi; singa, samaki mnono aliyejaa mafuta mwili mzima, nika, samaki mwenye nguzu za umeme ambaye kumshika lazima utumie mdomo wake wa chini vinginevyo utarushwa na kumwachia; kuvungwe, anayeitwa nguruwe wa majini kwa umbile na masharubu yake.


Ningependa pia kuwaona kungura, ndubu, kambale na wengineo. Sikuwa na bahati hiyo. Samaki niliowaona sokoni humo siku hiyo ni migebuka ambayo ilikuwa imekufa kwa








wingi. Ndubu? Siku hizi hapatikani sana. Kibonde? Alikuwepo mmoja tu leo, amegombewa kama mpira wa kona. Nikakata tamaa. Nikaenda soko la dagaa ambamo kulikuwa na dagaa wabichi wenyewe wakiwaita “mteke” na samaki wadogo wadogo walioitwa “Masembe.”


Nilipochoshwa na ziara hiyo nilitafuta hoteli na kuagiza chakula. Ningekula nini zaidi ya ugali wa muhogo kwa migebuka iliyokaangwa kwa mafuta ya mawese? Ulikuwa mlo mtamu uliofanya nijisikie shibe isiyo na kifani.


Baadaye nilipanda basi kwenda Ujiji. Sikujisikia kuondoka Kigoma bila kuuona mji huo wa kihistoria. Mji ambao ulikuwa na uzito mmoja na ile ya Bagamoyo, Zanzibar na Kilwa. Lakini mara niliposhuka kilima cha kutoka Mnarani na Mawemi matumaini yangu ya kuiona Ujiji inayosisimua ilizimika. Macho yangu yalipokelewa na mji wa kale, kama ulivyokuwa enzi za kina Tip Tippu na Livingstone.



Mji uliomezwa na nyumba nyingi ambazo ziliezekwa kwa nyasi au bati kuukuu. Baadhi ya nyumba zilikuwa kuukuu zikiashiria jambo lilelile ambalo nimekuwa nikiliona huku na huko toka nilipotoka kifungoni; Umasikini.


Hali ya mitaa mingi pia ilitia huzuni. Kwa mtu aliyetoka katika miji inayokua, hata Mwanga tu, Ujiji ingeweza kumtoa machozi. Mitaa mingi ilimezwa na majani. Baadhi ya mitaa majirani walianza kulima mahindi na maharage. Kuna nini? Nilijiuliza. Yako wapi magari yachangamshe mitaa? Wako wapi watu waitie uhai? Nini kimetokea hapa?


Nikafikia uamuzi. Bila shaka biashara ya utumwa ilikuwa na laana. Vinginevyo mji huu ambao Dakta Livingstone alitia kambi miaka ya 1871 wakati akifanya utafiti katika nchi za Kongo na Malawi. Mji ambao Novemba 10, mwaka huohuo








Henry Stanley, baada ya kutumwa kumtafuta alikutana naye ufukweni na kusEma “Dr livingstone…! I presume…” mwaka mmoja kabla ya kifo chake. Ukiwa njia na kituo kuu cha wafanyabiashara wa Arabuni, Ulaya na Amerika katika kujipatia bidhaa za meno ya tembo na ile biashara haramu ya watumwa. Mji ambao huwezi kuandika historia ya Afrika bila ya kuutaja! Hadi leo uko hivi! Kama si laana ni nini?


Nilishuka kwenye basi, nikaifuata barabara ya Livingstone ambayo ilinifikisha Pwani ya Ujiji, pale Livingstone alipokutana na Stanley kwa mara ya kwanza. Palijengwa nguzo ya kumbukumbu yenye maelezo ya hafla yao ile. Nikatupa macho yangu ziwani na kuziona boti za jahazi ya wavuvi waliokuwa katika pilikapilika za safari, ama kuondoka ama ndio kwanza wanafika toka maeneo hayo mbalimbali ya ndani na nje ya nchi.


Nikarejea Mwanga na kuanza kutafuta hoteli ya kulala. Ujiji haikuwa na nyumba ya aina hiyo. “Nenda Mwanga… nenda Kigoma mjini. Hapa utalala nje bure,” niliambiwa na msamaria mwema, mtu mzima aliyevaa kanzu na baragashia. Mkewe alivalia baibui lililomfunika gubigubi isipokuwa sehemu ndogo ya macho na miguu. Wazee hao walinikumbusha Bagamoyo na Pangani.


Wakati azana ya kuwakumbusha waumini kuwasili zinaanza kutoka misikiti mbalimbali mimi nilikuwa nikipanda basi kurudi Mwanga.




Hirizi Iliyopotea Na Maajabu Yake


SURA YA ISHIRINI NA SITA






engine kwa ajili ya safari ndefu ya wima toka Dar es Salaam, pengine kwa ajili ya chumba murua chenye hewa safi nilicholala nilijikuta


nimechelewa kuamka. Hivyo, basi la Mwarabu liliniacha. Nilioga harakaharaka, nikanywa chai kwa dagaa wa mteke, kisha huyoo, nikawahi malori ya mizigo. Nilipata moja lililokuwa likipakia mabati na vifaa vingine vya ujenzi. Kwa namna ya muujiza nilipata kiti cha mbele, tukiwa abiria wawili tu na dereva. Muda mfupi baadaye gari liliondoka.


Nikiwa nimekaa dirishani nilipata fursa nzuri ya kutazama nje, macho yangu yalivutwa na ardhi nyekundu, mimea ya asili, mashamba ya wenyeji na zaidi ya yote watu. Toka Mwanga hadi Gungu na baadaye Mwandiga yalikuwa maeneo ya watu, nyumba ambazo hazikutofautiana sana na zile za Mwanga na Ujiji. Hii hapa ikiwa imejengwa kwa saruji bati na samani nyingine zikiwa zimeipamba; ile ikiwa nyumba ya tope, ilijengwa kwa matete na mianzi na kuezekwa kwa nyasi.


Toka Mwandinga mambo yalibadilika zaidi. Nyumba duni zilianza kutamalaki huku zile za afadhali zikizidi kupungua. Watu pia walibadilika. Wengi walivalia mavazi








duni, baadhi yakiwa yamechanikachanika. Ilikua rahisi sana kumshuku mtu kuwa ni mwendawazimu kutokana na hali hiyo. Lakini pale unapoona idadi kubwa zaidi iko katika hali hiyo, hasa watoto ambao wengi wao walitembea nusu watupu, miguu iliyojaa vumbi jekundu ikiwa pekupeku, unajikuta ukiondokana na wazo lako na kupata jibu mara moja, rahisi; umasikini.


Nyuso za watu wengi zilionyesha dalili ya kukata tamaa. Walicheka ndio, lakini kicheko hicho kilionekana mdomoni tu, moyoni ungeweza kusoma kitu kingine kabisa. Walizungumza pale ulipozungumza nao, lakini sauti zao ziliashiria kuifadhi jambo fulani ambalo hawakuwa na uwezo wa kulifafanua. Sura hizi za msiba, majengo mengi ya maombolezo na ardhi nzuri ambayo haikuwa ikichekelea kwa pamba na kahawa kama nilivyoizowea utotoni ni jambo ambalo lilinitia hofu badala ya shahuku ya kufika nyumbani. Nilihisi huzuni ikinigubika katika fikra zangu katika safari hiyo nzima.




Ndiyo, nchi yetu ni masikini. Lakini umasikini huu unazidiana kati ya mkoa na mkoa. Pengine iko mikoa iliyo taabanizaidi ya Kigoma, hilo halikunisumbua. Kilichonisumbua ni kwa nini Kigoma iwe katika kundi hilo? Kigoma haikuwa na sababu yoyote ya kuwa kama ilivyo. Ni mkoa uliojaaliwa kila ambacho binadamu anahitaji. Ardhi ilikuwa na rutuba tele, mali asili zikiwa zimefurika katika misitu na ardhini. Mito, mabwawa na baba lao; ziwa Tanganyika vikiwa vimejaa samaki tele ambao ladha yake ina uwezo wa kumshangaza mtu yeyote duniani zaidi ya hiyo Kigoma ni lango muhimu kwa nchi za Kongo, Burundi na hata Zambia. Ukweli huo pekee wa kijiografia ni rasilimali tosha. Historia ya Kigoma, hasa Ujiji pia ni rasimali nyingine muhimu ambayo kuitumia vyema








kungeweza kuubadili mkoa kiuchumi.


Kitu gani kimetokea hata mkoa uwe ukirudi nyuma badala ya kwenda mbele? Kitu gani kimesahauliwa? Nani alaumiwe? Nilijiuliza hili na lile. Yako mengi ambayo hayakuhitaji utafiti wa kina kuyaona. Moja la haraka likiwa usafiri. Ilikuwa rahisi zaidi kutoka Kigoma kwenda Burundi au Kongo kuliko kwenda Tabora au Mwanza, achilia mbali Dar es Salaam. Wakati huu wa Kilimanajaro au Arusha anaweza kutoka Dar es Salaam hadi kwao na akarudi jioni au kesho yake ilimchukua mtu wa Kigoma wiki mbili au zaidi kufanya safari hiyo, hali ambayo muuza nyanya au samaki ataishia kuiona bidhaa yake ikioza mbele ya macho yake.


Barabara ilikuwa tatizo la kwanza lisilohitaji mjadala barabara pia lilikuwa tatizo la pili. Kigoma ulikuwa mmoja kati ya mikoa iliyo kimya sana. Pamoja na kukisiwa kuwa na eneo la kilometa za mraba 37,037 mkoa wa Kigoma ulikuwa hauna kiwanda hata kimoja. Hata wale samaki, aina ya migebuka ambao katika misimu fulani huliwa kwa mamilioni huishia kuharibika bure na kutupwa badala ya kusindikwa; achilia mbali dagaa wanono wenye sifa zote.


Hata mafuta ya mawese, yatokanayo na michikichi ambalo ni zao linalostawi sana mkoani humu hayajapata kujengewa kiwanda cha kuyasindika ili yauzwe kimataifa. Nani atafikiria kufanya mradi kama huo mahala ambapo hakuna hata barabara?



Barabara pekee ambayo haikuaminika sana ya kutoka Kigoma kwenda nje ya mkoa na hiyo tuliyokuwa tukiitumia. Sehemu ndogo sana zilikuwa na lami. Sehemu kubwa ikiwa changarawe na tope ambalo lilifanya safari iwe shughuli kubwa badala ya starehe. Lakini hilo halikuwa tatizo kubwa.








Tatizo hasa lilikuwa mzunguko wa njia hiyo ulioifanya kuwa ndefu kupita kiasi. Ili kwenda Dar es Salaam au Tabora miji iliyoko mashariki ya mkoa ulilazimika kwenda kaskazini, upite Kasulu, Kibondo hadi Biharamulo kabla hujageuka kuelekea kusini ili ufike Kahama na Nzega kabla ya kuingia Tabora. Toka Tabora unapanda kaskazini tena na kuridi Nzega kabla ya kwenda Igunga, Iramba, Singida hadi Manyoni. Toka hapo utafika Dodoma na kutelezea Gairo, Morogoro, Chalinze na baadaye Dar es Salaam! Pema hapo?


Ndiyo, Kigoma kuna uwanja mdogo wa ndege. Ndege ndogondogo vilevile huja na kuondoka mara mbili au tatu kwa wiki. Licha ya ukweli kuwa hazitoshi, bado nauli kubwa ya ndege imefanya ziwe na wenyewe badala ya kila mtu. Si kila mtu mwenye laki mbili au tatu kwa safari ya saa nne kwenda na kurudi.


“Vipi unashukia wapi?” dereva alinizindua. “Naona uko mbali sana kimawazo,” aliongeza.


Nikapekecha macho yangu kwa kidole change cha shahada kabla ya kumuuliza, “Kwani hapa ni wapi?”


“Tumeshapita Simbo. Hapa ni Kitawe. Baada ya hapa tunaingia Mayange. Toka hapo ni moja kwa moja hadi Kasulu, mwisho wa safari yetu.”


Sikujua nimjibu nini. Kwa kweli, sikujua hata mahala pa kushuka. Niliondoka nikiwa mdogo sana. Kumbukumbu nilizokuwa nazo zilionyesha kuwa hatukuwa mbali sana na mji wa Kasulu. Lakini udogo, mabadiliko makubwa ya mazingira na hasa kutoweka kwa misitu mingi ambayo ningeweza kuikumbuka kulifanya nisijue wapi pa kuanzia upelelezi wangu wa kutafuta chochote nitakachoweza kupata juu ya wazazi wangu.








Nadhani dereva alizisoma hisia zangu. Kwani alirahisisha kazi yangu pale alipouliza, “Yaelekea wewe ni mgeni sana huku?”



“Nadhani, maana niliondoka nikiwa mdogo sana. Hata sifahamu nianzie wapi kuwatafuta wazee wangu,” niliropoka bila kutegemea.


Kwa wakazi wa mkoa ambao hauna ajira za kutosha, ambao mkoloni aliutumia kama shamba la kuchukulia manamba wakakate mkonge huko Tanga na Kilimanjaro maelezo yangu hayakumshangaza dereva huyo hata kidogo. Alihitaji maelezo mafupi tu; niliondoka lini. Tulikuwa tukiishi wapi, ukoo wangu ni upi na mengineyo. Nilipomweleza juu ya hofu yangu juu ya vijiji vya Ujamaa alinielewa mara moja. Akanishauri nishuke katika kijiji kinachofuata, kinachoitwa Mayange, ambacho ni kikubwa na kilikusanya familia mbalimbali toka maeneo mengi.


“Walisema kingekuwa kijiji cha mfano kwa maendeleo,” alisema akicheka kwa kebehi. “Hebu katazame hayo maendeleo halafu utatuambia.”


na ushauri wake. Tulipofika Mayenge nililipa nauli yangu, nikateremka na kuanza kazi ya kutafuta ‘kwetu’.


Kama nilivyotegemea kijiji cha Mayange kilikuwa kinyume kabisa na matarajio ya awali kama ilivyokuwa kwa vijiji vingine vyote tulivyovipita njiani, Mayange ilitoa taswira ileile, umasikini unaonuka. Karibu watoto wote walichakaa miili na mavazi, wakifanya kazi ndogondogo kama kubeba mizigo ya wasafiri kwa mikokoteni yao ya miti au kuomba tu kwa wapita njia. Baadhi walivaa sare za shule. Lakini sare nyingi kati ya hizo hazikufanana kabisa na malengo ya wizara








kwa kuchoka na kuchakaa.


Watu wazima nao walikuwa na yao. Wengi wao walikuwa taabani, suruali zikiwa zimejaa viraka, shati zikiwa zimepasukapasuka, miguu iliyokuwa peku ikiwa imebadilika rangi kutokana na vumbi jekundu lililowapiga pindi wakihangaikia mkono kwenda kinywani.


Waliahidiwa huduma muhimu kama barabara; hazikupata kujengwa au kukarabatiwa. Waliahidiwa maji ya bomba; hawakupata kuyaona. Waliahidiwa umeme; ilikuwa ndoto za mchana. Waliahidiwa huduma ya matibabu; sasa ilibidi kuyalipia kwa fedha ambazo huna. Kwa ujumla, ahadi zote zilizotumiwa ili kuwaondoa katika makazi ya baba na babu zao ziligeuka hewa. Jambo hilo lilifanya nyuso za kila mtu unayekutana naye zitangaze dalili zote za kukata tamaa.




Kazi ya kuitafuta familia moja, kati ya familia zaidi ya mia saba zilizohamishiwa hapo toka maeneo tofauti haikuwa ndogo. Nilitumia zaidi ya saa mbili kabla ya kumpata mzee mmoja ambaye alimfahamu babu, “Familia ya Kionambali, sio? Wala usihangaike. Wako humuhumu. Mtoto wake Karimanzira huwa namwona mara kwa mara.”


Nikapata matumaini. “Ni babu? Kionambali mwenyewe?” niliuliza.


“Huyo sina habari zake. Sijui kama bado yuko hai au tayari ametangulia,” mzee alinijibu. Laiti angejua kauli yake ilivyonishtua.


Nikiwa na matumaini mapya nilianza awamu ya pili ya kuwatafuta wazazi wangu. Zikiwa safari za mguu, katika kijiji kikubwa kisicho walao na jina la mtaa ilinichukua saa moja na nusu kabla ya kuonyeshwa kwa mbali nyumba iliyoaminika kuwa ya baba.








Ilikuwa nyumba iliyofanana na nyingine nyingi kijijini hapo; tofali za tope ambazo zilichakaa kabla ya kupata lipu, achilia mbali rangi. Juu nusu iliezekwa bati kuu kuu nusu nyasi. Sakafu ilikuwa ardhi ileile waliyoikuta palepale.


Nje ya nyumba hiyo alikuwepo bibi mmoja mchovu kama wengine wote kijijini hapo, akisuka ukili. Nilisogelea na kumwamkia. Kisha niliuliza kama hapo palikuwa nyumbani pa mzee Karimanzira. Swali langu lilimfanya bi mkubwa huyo ainuke na kunitazama kwa makini. Mara nikamwona akianza kutetemeka. Machozi yakianza kumtoka.


“Wewe ni Mtukwao!... Mwanangu! Umerudi…” alisema akinijia na kunikumbatia kwa nguzu zake zote.


Alikuwa mama! Mama yangu kipenzi! Fuko nililokuwa nalo mkononi lilidondoka pwaa, mikono yangu pia ikamkumbatia kwa nguvu. Masikioni nilisikia sauti nzito ya kiume ikilia! Kilio cha kwikwi. Ilinichukua muda kubaini kuwa ilikuwa ni mimi niliyekuwa nikilia.


Mara mzee mmoja akatoka nje ya nyumba hiyo. Alikuwa mchovu vilevile. Umbile lake refu lilipinda kwa mbele, ndevu zenye mchanganyiko na mvi zilimeza kidevu na kichwa chake kizima. Akitetemeka miguu na mikono yeye pia alinijia na kunikumbatia, machozi yakimlengalenga.


Baba! Amezeeka kabla hajapata kuwa kijana!


Dakika mbili tatu baadaye nyumbani palifurika. Watu waliotoka huko na huko walijazana kushangilia ujio wangu. Kila mtu alisema lake, ingawa mada ilikuwa ileile; Mwana mpotevu karejea!


Niliingizwa ndani, nikapewa kiti cha kifalme; kigoda cha baba. Fumba fumbua togwa tamu ikaletwa. Nikapewa kata kubwa iliyojaa. Kabla haijaisha nililetewa mihogo mitamu,






huko nje nikiwaona vijana wakikimbizana na jogoo.


Baba na mama hawakubanduka ubavuni mwangu. Walikuwa na mengi ya kuniuliza mengi ya kunisimulia. Kwa bahati mbaya, hali haikuruhusu. Watu walikuwa tele, wakinishangaa kana kwamba nimetoka mwezini. Kelele pia zilishamiri. Watoto ambao hata sikuwafahamu walijipenyeza na kukaa miguuni mwangu, wakijitahidi sana kunikumbatia, walao miguu.


Kwa kweli sikutarajia mapokezi makubwa kama haya. Nikiwa mtu aliyepotea kwa zaidi ya miaka thelathini, mtu aliyerudi akiwa mikono mitupu kama nilivyokuwa, nilitarajia kupokelewa kwa kejeli au dharau. Si vicheko na kushangiliwa kwa takribani kijiji kizima kama ilivyokuwa. Hata hivyo, nilijihisi kama mtu aliyeutua mzigo mzito uliomlemea. Nilijihisi kama ambaye nilifutiwa madhambi yangu yote hata kabla ya kuomba radhi.


Kitu kimoja tu kilikuwa kikinisumbua. Mtu niliyetamani kumwona pengine kabla ya wengine wote hakuwa katika kundi la watu waliojitokeza kunilaki. Mtu huyohuyo nilihitaji sana kumwomba radhi kwa kumwamgusha katika matarajio aliyokuwa nayo juu yangu na kumpotezea hirizi yake muhimu. Nilimtegemea awe katika mjumuiko huo, aniite kando ambako tungeketi peke yetu na kuteta kama mtu na baba yake. Sikumwona. Wala sikuthubutu kuuliza harakaharaka kwa kuchelea kupewa jibu ambalo lingeweza kunitia ugonjwa wa moyo; Babu yake! Mbona alikufa zamani?


Kuku alikwishachinjwa na kupikwa. Ugali mweusi wa nyangwe uliletwa mbele yangu kwa kitoweo cha kuku huyo. Bila kuambiwa wageni walianza kupungua ili kuniachia faragha ya kufaidi chakula changu. Nilishindwa kujizuia. Kabla








ya kumega tonge la kwanza nilimuuliza baba, “Babu yuko wapi?” nilisubiri jibu lake kwa hofu kubwa, moyo ukinidunda. Lakini nilipomwona baba akitabasamu kabla hajanijibu hofu ilitoweka moyoni mwangu.


“Babu yako kwani humjui?” baba alisema. “Aligoma katakata kuhama. Jeshi la polisi, jeshi la mgambo na hata sungusungu walishindwa kabisa kumtoa. Hivi sasa yuko peke yake ndani ya msitu mkubwa wa yaliyokuwa makazi yake. Kila wiki huwa nakwenda kumjulia hali.”



Nikapumua. “Bibi?” niliuliza.


“Yeye hatuko naye tena. Alitutoka miaka mitatu iliyopita. Alipatwa na ugonjwa wa malale uliokataa kila aina ya dawa.”


Ladha ya kuku ikaniishia palepale.




***


“Nilijua utarudi salama… nilikuwa nikikusubiri… nisingeweza kufa kabla hujarudi, mjukuu wangu,” ilikuwa kauli ya kwanza ya babu mara aliponitia machoni na kunipapasa kichwani.


Sikuweza kuyastahimili machozi yaliyomiminika toka machoni mwangu. Babu alinikumbatia, huku mkono wake ukiendelea kunipapasa kichwani kwa namna ya kunibembeleza. Kitendo hicho kilizidisha uchungu moyoni mwangu na kunifanya nizidi kulia. Kwa mara ya kwanza, hakunishutumu kwa kitendo hicho. Niliinua uso na kumtazama kwa wizi. Yeye pia alilowa macho kwa machozi.


Babu analia, chuma cha pua!


Kwangu, alikuwa zaidi ya babu. Alikuwa kila kitu; baba, babu, rafiki, mwalimu na zaidi ya hayo. Hayo nilibaini na kuyahakikisha muda huo ambao mzee hataweza kustahimili








kabisa kuficha udhaifu wake kwangu! Nitamsimuliaje malaika huyu kuwa jitihada zake zote za kupita mabonde, milima na misitu yenye hatari zote za dunia, hadi kunifikisha nchi ya Wahaya ili nipate elimu zilikuwa kazi bure? Nitaanzaje kumwambia kuwa ile hirizi yake, urithi pekee alioniachia ilipotea kwa uzembe? Niliteseka vibaya sana akilini nilipowaza hayo.


Nilikuwa nimemlazimisha baba alfajiri tu ya siku iliyofuata aniongoze kuja kumwona babu. Yeye akisisitiza kuwa ningepumzika walao siku mbili kabla ya kufanya safari hiyo. Jambo ambalo sikuafikiana nalo.


Kwa kutokuwa na uhakika wa kuwapata wazazi wangu, wakiwa hai nilifika nyumbani mikono mitupu. Hivyo, nilipopata fursa ya faragha ya kumkabidhi baba shilingi 50,000 kati ya zile laki moja nilizobakiwa nazo nilionekana shujaa mkubwa. Baba alianza mipango ya ‘kumaliza bati’ mama aliongea juu ya kulimisha shamba. Ilikuwa kama nimetoa milioni hamsini. Tulimkuta babu akifunga mbuzi wake nje ya nyumba.






Alivaa nguo zake zile alizozipenda, kaptula na shati nyeupe. Ziling’ara kama nilivyoziacha! Miguuni alitilia buti zake ambazo nazo ziling’ara kwa kiwi, ingawa zilianza kuchoka. Alikuwa peke yake katikati ya pori, isipokuwa kwa mifugo mingi ya mbuzi, kuku na bata. Watu wa pwani wangeweza kuapa kuwa ni jini jeupe linalokaa peke yake msituni. Babu alikuwa ametusikia toka mbali. Hivyo, alimfunga mbuzi yule harakaharaka na kusimama akitukodolea macho. Alipotuona alitukimbilia na kunidaka juujuu. Angeweza kunibeba… angeweza kunitia mweleka…. Babu alikuwa na nguvu zake. Ilikuwa kama ni binadamu pekee aliyebishana na uzee. Binadamu ambaye hakukubali kusalimu amri kwa kifo.








Pamoja na baba tulikuwa na vijana wengine wawili ambao nilielekezwa kuwa ni ndugu zangu. Vijana hao walipewa amri ya kumkamata beberu mkubwa kuliko wote na kumchinja. Akachunwa. Moto ukawashwa. Muda mfupi baadaye, tulikuwa tukimla mbuzi yule, wa kuchoma. Babu, akiwa na meno yake yote alitafuna mguu mzima wakati wengine tukishika shika hapa na pale.


Baadaye babu aliwataka baba na wale wenzetu wengine kuondoka kwa maelezo kuwa alikuwa na mengi ya kuzungumza na mjuu wake faragha. Usiri wangu na babu halikuwa jambo geni kwa baba, toka utoto wangu. Hivyo, hakutia ubishi, walichukua nyama ya kula nyumbani wakaondoka zao kwa ahadi ya kunifuata kesho.


Nikapata wasaa wa kuchomoa zile elfu hamsini nilizobakiza na kumkabidhi babu. “Zawadi pekee niliyoweza kukuletea ni hii,” nilisema kwa masikitiko.


Babu hakuzipokea. Badala yake alicheka kabla ya kusema, “Sidhani kama nazihitaji. Za nini? Kaa nazo, zitakufaa wewe zaidi. Naamini bado unasafari nyingine ndefu, yenye mafanikio makubwa zaidi. Halafu, bado tuna mengi ya kuzungumza, mimi na wewe.”




“Bila shaka. Niliitikia.


“Miaka mingapi vile toka tumetengana?” Babu aliniuliza. “Mingi sana. Ni aibu kuitaja.” Nilimjibu.


“Aibu ya nini? Mwanaume anayeonea aibu masaibu yake hafai. Kwa nini ufanye jambo ambalo utalijutia maishani mwako?”


Nilijua darasa la babu limeanza. Sikuwa tayari kwa darasa lolote wala somo lolote kabla ya kumtaka radhi. Hivyo nikajikongoja na kumwambia, “Babu ningeomba nianze kwa kukutaka radhi.”








“Radhi ya nini?” “Hirizi.” “Ilifanyaje?” “Ilipotea!”


Nilitarajia babu abadilike, akasirike. Lakini kwa mshangao nilimwona akiachia tabasamu jembamba. “Nisubiri kidogo,” alisema akiinuka na kuingia ndani, aliporejea alikuwa na hirizi mkononi.


“Hirizi hii siyo?”


Niliitazama kwa makini. Nisingeweza kuisahau. Ilikuwa




ileile!






Sikuyaamini macho yangu. Nikamkodolea babu macho




ya mshangao.


“Hii ndiyo inayokusumbua?” babu aliongeza baada ya kicheko kingine. “Usiwe na wasiwasi. Ilipotea ikatafuta njia, ikarudi nyumbani kukusubiri.”


Bado sikuweza kuelewa. Hirizi hiyo ilipotea porini katika purukushani za kuikimbiza isianguke mikononi mwa padri. Yule kimbelembele, Byabato, alinihakikishia kuwa aliiokota tena na kumrudishia padri Backhove ambaye aliichoma, ikakataa kuungua. Kwamba baadaye ilitupwa baharini. “Ilifikaje kwako?” nikamuuliza.


“Ni hadithi ndefu. Ili kuifanya fupi pengine nikuambie tu kuwa ililetwa.”


“Na nani?” nilizidi kumbana babu. “Na mizimu ya babu zetu.”


Bado nilikuwa sijamwelewa. Nikamwambia hivyo. “Mizimu ina njia nyingi ya kuwalinda wahanga wake,”


alifafanua. “Chochote kilichokutokea hadi hirizi hii kutengana nawe wahanga walikuwa wakiona. Ama kwa kujigeuza ndege,








ama kwa kuwatuma ndege, hirizi hii ililetwa hadi katika mikono yangu.”


Babu alipoona kuwa bado sijaridhika na ufafanuzi huo aliamua kuwa wazi zaidi. Alisema kuwa jioni moja alikuwa akiwinda katika mwambao wa mto Malagalasi. Mara akaona kundi kubwa la ndege aina ya hondohondo wakitua hatua chache toka alipokuwa. “Walikuwa wengi. Kama elfu moja hivi. Waliponiona waliruka kunikimbia. Lakini mwenzao mmoja hakuweza kuruka. Alikuwa akipigapiga mabawa kwa nia ya kupaa lakini hakuweza. Nikamsogelea kuona kapatwa na nini. Nikabaini kuwa shingo yake ilikabwa na kamba nyeusi ambayo ilinasa kwenye kichaka cha mti. Nilipomshika ili kumkwamua ile kamba nilishangaa kuona kuwa ilikuwa hirizi ile niliyokupa. Nikaitoa na kumwacha ndege ambaye alipaa kuwaendea wenzake waliokuwa wakihangaika angani kumsubiri.”


Ilikuwa habari ya ajabu kwangu. Hirizi yangu, iliyopotea zaidi ya miaka thelathini iliyopita imerejea mikononi mwangu. Niliipokea, nikaipapasa. Ilikuwa ileile, kwa rangi na uzito. Kwamba imerudi mikononi mwangu halikuwa jambo la ajabu sana, ni namna iliyoifanya irudi ambayo kichwa changu hakikuweza kupokea.


Falsafa nyingi zilipita kichwani mwangu. Kama kweli ilitupwa ziwani bila shaka ingeweza kuoza. Kama hilo halikutokea ni wazi kuwa ilimezwa na samaki ambaye huenda alivuliwa na kuliwa. Kama ilikuwa hivyo hirizi itakuwa ilitupwa kama sehemu ya uchafu wa matumbo ya samaki wanayotayarishwa kwa ajili ya minofu kusafirishwa Ulaya na “mapanki” kuvamiwa na akina baba na mama ntilie. Inawezekana kuwa katika jitihada za kujitafutia chochote ndege yule alijikuta ameivaa hirizi ile na kuisafirisha bila








kujua? Kama ni kweli kwa nini ailete hadi miguuni mwa babu? Katika pitiapitia yangu vitabuni nilikuwa nimesoma mahala tabia za ndege. Moja ya tabia zao za ajabu ni ile ya kuhama au kusafiri safari za mbali kila ifikapo msimu fulani. Mara nyingi ndege hao wanaweza kusafiri safari za mbali toka Marekani au Ulaya hadi Afrika. Inaaminika kuwa wengi uhama katika vipindi vya hali fulani ya hewa na kurudi hali inapotengemaa. Inaaminika pia huko ambako huenda ndiko ambako ndege huzaliana na kurejea likiwa kundi kubwa zaidi. Inawezekana kabisa kuwa hondohondo aliyebeba hirizi yangu alikuwa katika msafara huo. Anaweza kuwa alikuwa akitoka


zake Ulaya au nchi za Kiarabu na kuelekea Afrika Kusini!


Babau alikuwa kama anayeyasoma mawazo yangu. Alikohoa kidogo kabla ya kusema, “Naona na wewe tayari umeambukizwa yale maradhi yenu.”


“Maradhi gani?


“Maradhi ya kisomi. Naona unavyoona shida kuamini kuwa mizimu ya babu wa babu zako imekurejeshea hirizi hii! shauri lako. La msingi ni kwamba hirizi yako imerejea na tangu leo utaivaa tena. safari hii milango yote uliyoshindwa kuifunguwa itafunguka,” alisema akinivisha hirizi hiyo na kisha kunitemea mate kichwani na kifuani.


“Kuna jambo la pili.” Alisema akiinuka tena na kurudi ndani. Aliporejea alikuwa na bahasha tatu mkononi. Alinikadhi. Ilikuwa barua. Juu ziliandikwa jina lake na anuani ya kiji chake. Ilielekea barua hizo zilitoka nje ya nchi, kwani stempu zote zilikuwa na picha ya malkia au wafalme wazungu, muhuri ukiosomeka waziwazi “Stockholm-sweden”. Tarehe kwenye mihuri hiyo zilionyesha kuwa zilitumwa zaidi ya miaka kumi na mitano iliyopita!








“Barua!” Niliropoka.


“Ndiyo,” babu alijibu “Mbona hazijafunguliwa? Ni za zamani sana,” nilisaili.


Babu naye akaonyesha mshangao wake kwangu, “Mjukuu wangu, zinalekea kuwa ni barua muhimu sana. Unadhani ningeweza kumpelekea mtu yeyote asome siri zangu na kuanza kunitangaza? Nilikuwa nakusubiri, nilijua ungerudi salama.”


“Ni wewe peke yako utakayekuwa wa kwanza kuelewa chochote kilichoandikwa humo.”


“Zilifikaje hapa?” Niliuliza nikianza kufungua moja


niliyoiona ya zamani zaidi.


“Zililetwa. DC alileta kwa mkono wakemwenyewe.


Alinishawishi kufungua lakini nilikataa katakata.”


Baada ya maelezo hayo babu alikunjua kiti chake cha uvivu, kilichotengenezwa kwa ngozi ya nyati na kujilaza kimya kwa namna ya kunipa wasaa wa kusoma barua hizo kwa tuo. Barua ya kwanza ilikua ndefu kidogo. Ilianza kwa salamu za siku nyingi, ikaendelea kwa taarifa ya kuipongeza kazi yake alipokuwa nchini humo, “Tumetengeneza filamu mbili za ile michezo uliyoshiriki kuicheza. Filamu hizo zimependwa sana Ulaya nzima zinanunuliwa kama peremende. Taarifa tuliyoichapisha hapa chini ni malipo yako ya mrabaha hadi sasa. Tunaomba ufanye kila uwezalo kuwasiliana nasi ili


upokee malipo yako,” ilieleza barua hiyo.


Sehemu ya pili ya barua hiyo ilikuwa na mahesabu ya idadi ya mikanda iliyouzwa na televisheni zilizonunua hakimiliki na hakishiriki. Kwa hesabu za harakaharaka asilimia ya babu ilionyesha kama dola 227,000. Sikuyaamini macho yangu. Nikainua macho kumtazama. Alikuwa amesinzia, tabasamu likiwa mdomoni.








Nikafungua barua ya pili. Hii iliandikwa mwaka mmoja baadaye. Ilisisitiza, umuhimu wa babu kwenda haraka au kumtuma mrithi wake yeyote anayeaminika. Iliongeza kuwa iwapo kuna tatizo lolote la vitambulisho mwakilishi huyo alichotakiwa ni kwenda na ile hirizi ambayo ilikuwa haibanduki shingoni mwake. “Benki yetu tayari imearifiwa juu ya hilo. Usiwe na wasiwasi,” iliongeza barua hiyo.


Barua ya tatu iliambatanishwa na hundi. Hesabu zilizoandikwa juu ya hundi hiyo zilinitatanisha dola 812,000! Barua ilisisitiza fedha hizo kuchukuliwa. Ikiongeza kuwa benki yao tayari imefungua matawi nchini katika miji ya Dar es Salaam na Mwanza, haikuwepo haja ya kusafiri hadi Ulaya tena.


Mara nikaanza kupata njozi za mchana. Nilijiona nikiandika kitabu, ambacho kiliyahusu maisha yangu mwenyewe. Niliyaumba na kuyaumbua matukio, mikasa na visa vyote vilivyonikumba toka katika safari zangu kuu mbili safari ya kimaisha iliyonifikisha kila pembe ya nchi na ile ya kimaumbile ambayo ilinitoa utotoni na kuniingiza ukubwani. Nilihisi hata jina la kitabu likinijia akilini; Kiguu na Njia.


Zikanijia njozi nyingine. Katika njozi hizi nilijiona nikiwalekeza watu wa masuala ya filamu wapi pa kuelekeza kamera zao, katika filamu niliyokua nikiitengeneza. Niliwataka ihusishe maeneo yote muhimu ya nchi yetu, mbuga za wanyama, maziwa na mito yote ambayo haikupata kutangazwa vizuri. Kwa njozi niliona mikanda ya filamu hiyo ikigombewa na kuwafanya watazamaji waone hazina kubwa iliyosahauliwa ambayo walijaliwa na Muumba.


Nikaona jinsi nilivyokuwa nikiishi na mke wangu Nashifa kwa furaha. Watoto wetu wawili wenye afya njema








wakicheka na kufurahi…


Halafu nikamkumbuka mwenye fedha zake, ambazo zingeniwezesha kufanikisha ndoto hiyo. Nikageuka.


“Babu!” niliita tena nikimtazama.


Alikuwa bado amelala vilevile kwenye kiti chake cha uvivu. Tabasamu lake lilikuwa bado limesahauliwa palepale usoni kama mtu aliyekuwa katika dimbwi la starehe. Niliinuka na kumshika bega. Nikamtikisa taratibu, baadaye kwa nguvu kidogo, “Babu… babu… babu…!


Kimya! Kimya!


Nikashtuka. Alikuwa kama hapumui! Nikamshika kifua kusikiliza mapigo ya moyo. Hayakuwepo. Hata mwili wake tayari ulikuwa umepoa. Ndio kwanza nikabaini kuwa babu hatukuwa naye tena duniani! Tabasamu lake lililobakia palepale kama ishara ya ushindi kwa jambo zito lililokuwa likimsumbua kwa muda mrefu.


Nilitetemeka mwili mzima. Nguvu zikaniishia, furaha, faraja na matumaini makubwa niliyoyapata mara baada ya kuisoma barua yake, ikatumbukia nyongo.


MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Blog