Search This Blog

Thursday 29 December 2022

MPANGO WA NJE NI PIGO BUTU LA KIFO - 2

   

Simulizi : Mpango Wa Nje   Ni Pigo Butu La Kifo

Sehemu Ya Pili (2)



"Ulijuaje au mlijuaje kama ni risasi na msihisi kitu kingine?" Akachomekea swali jingine Sembuyagi.




"Hata kama si wataalamu wa kujua risasi inaua vipi lakini kwenye mwili wa Gabriel hauhitaji mwalimu wa digirii ya utambuzi wa masuala hayo akujuze."




"Dokta hakuwa na ugomvi na mtu/watu au hata tabia za ukorofi hapa aishipo?"




"Si katika pambo la kumpamba marehemu tu lah! Ukweli uliowazi ni kwamba mzee Gabi alikuwa mcheshi mpenda vijana na mara nyingi hukaa pamoja nao hasa akiwa hana shughuli nyingi zilizomzonga. Hakuwa mtu wa purukushani za hovyo." Akajibu kijana yule wa kwanza akiwa katika utulivu. Jicho la Sembuyagi likatua mlangoni ambako aliwaona askari watatu wakiwa wanaingia na kutoka huku wengine wakiwa wanajaribu kupata ushahidi kutoka kwa waliyokaribu ama mashuhuda waliyowakuta. Akatamani afike kwenye ule mlango na kuuliza chochote hata hivyo hakutaka kuingilia majukumu ya wengine. Kwa mtazamo wa kawaida tu ni kwamba kesi hiyo ya mauaji ilishaingia kwenye mikono ya askari polisi. Yeye pia alikuwa na ulazima wa kujua sababu ya kifo cha Dokta huyo hata hivyo alipuuzia jambo hilo na kujipa utulivu. Akawaacha wale vijana pasipo kuwaaga akapiga hatua hadi mbele kidogo na kuwakuta wakinamama wakiwa wanaongea wanayoyajua na wasiyoyajua akasikiliza kidogo na kuzidi kusonga mbele alishawapanga vijana wake kila kona ili kuona kama anaweza kupata kitu ama kuona mtu watakaye mtilia shaka. Akilini mwake alikuwa akimuwaza yule mtu aliyefika ofisini kwa Daktari huyo mchana. Aliamini kwa asilimia zote angeweza kuwa hapo kutokana na tukio hilo la kuuawa kwa Dokta Nyagile. Muda ukakatika na mtu huyo aliyetarajia kumuona asimuone. Kila alipozitazama sura za watu waliyoko hapo hakuweza kuona hata sura moja yenye kuitilia mashaka.




___________




Nilivyokurupuka asubuhi alijua Mungu ama Malaika wake, sikutaka kusikiliza chochote wala kusoma chochote, nilitazama saa yangu ya ukutani ikaniambia tayari ilikuwa ni saa mbili kamili asubuhi. Sikupoteza wakati nilijiandaa na kisha nikatoka na kuifunga nyumba imara nikaingia mjini. Nilifika masika kisha nikalielekea jengo moja kubwa nikapiga honi mara moja lango likafunguliwa baada ya kusubiri kwa muda fulani. Niliingiza gari ndani ya uzio wa jengo hilo kisha nikaelekea hadi kwenye maegesho ya magari nikaegesha gari nikashuka. Nilimsalimia mlinzi ambaye alinifungulia lango hilo kisha nikauelekea mlango mkubwa wa kuingia ndani nikaufungua na kuufunga nyuma yangu. Jengo hili lilikuwa likiishi wapangaji wengi tu na lilikuwa ni jengo linalomilikiwa na kitengo chetu cha ujasusi hata hivyo hakukuwa na mtu aliyejua kama jengo hili wamiliki ni sisi bali wapangaji wengi walijua kuwa hata sisi ni wapangaji. Gari zilikuwa zikiegeshwa mahala pamoja hivyo ikawa ni ngumu kutilia shaka na sidhani kama kulikuwa na mtu ambaye alitaka kujua hilo. Nilipoingia nilizifuata ngazi zilizokuwa zikielekea ghorofa ya pili nikazipanda hadi ghorofa ya pili nikaifuata koridi ndefu ambayo ilikuwa inamilango isiyopungua sita mitatu kulia na mitatu kushoto. Nikapiga hatua zangu hadi kwenye mlango wa katikati au wa pili kulia nikatia funguo zangu na kuingia ndani. Korido hii ya upande huu niliyopo ilikuwa ikimilikiwa na kitengo chetu na vyumba hivi sita vyote vilikuwa vikimilikiwa nasi, vyumba vya upande wa kulia vilikuwa ni ofisi ndogo ndogo na sehemu ya mazungumzo na mipango myepesi ihusuyo shughuli zetu za kijasusi na vyumba vya kupumzikia vya muda kama mtu miongoni mwetu atapenda na muda mwingine maeneo haya tunayatumia kama maficho kwa mtu muhimu kwetu tusiyependa aonekane na macho ya watu. Vyumba vya upande wa kushoto ilikuwa ni njia moja tu ya kutokea kwenye chumba kikubwa sana ghorofa ya chini ambacho kilitumika kuegeshea magari yanayomilikiwa na kitengo chetu cha ujasusi. Mtu anapoingia chumba cha kwanza kushoto ni lazima atatokea kwenye chumba cha pili kushoto na atakayeingia chumba cha tatu kushoto hana tofauti na aliyeingia chumba cha kwanza kushoto. Nilipofika ndani ya chumba hicho nilikutana na seti ya Sofa yenye makochi matatu mawili ya watu wawili wawili huku moja likiwa na uwezo wa kubeba watu wane. Kulikuwa na kabati kubwa na pana la ukutani mbele ukiingia tu ndani ya chumba hicho, kushoto kwenye kona kukiwa na friji kubwa la kioo ambalo lilijaa vinywaji vikali. Kilikuwa ni kama chumba cha kupumzikia ama sebule fulani kwa namna kilivyokaa, hatua kama tatu mkono wangu wa kushoto kulikuwa na meza pana ya duara yenye kioo cheusi kinene ambacho kwa juu kilikuwa na pakiti ya sigara Embassy na kiberiti cha gesi. Nikatabasamu baada ya kujua mtumiaji wa bidhaa hiyo ni nani hata hivyo ilikuwa asubuhi sana sina shaka mtumiaji alitumia mwishoni mwa siku iliyoisha.








Kilikuwa ni kama chumba cha kupumzikia ama sebule fulani kwa namna kilivyokaa, hatua kama tatu mkono wangu wa kushoto kulikuwa na meza pana ya duara yenye kioo cheusi kinene ambacho kwa juu kilikuwa na pakiti ya sigara Embassy na kiberiti cha gesi. Nikatabasamu baada ya kujua mtumiaji wa bidhaa hiyo ni nani hata hivyo ilikuwa asubuhi sana sina shaka mtumiaji alitumia mwishoni mwa siku iliyoisha. Sikuwa na muda wa kupoteza hapo nililifuata kabati mbele yangu kisha nikatia ufunguo mmoja kutoka kwenye kikasha cha funguo nyingi za milango tofauti. Mlango wa kabati ukafunguka kwa msaada wa mkono wangu baada ya kuuvutia kwangu. Lilikuwa tupu kabisa hili kabati macho yangu hayakukutana na kitu kingine chochote zaidi ya kifaa kilichobeba vitufe viwili tu kimoja kikiwa na rangi nyekundu na kingine kikiwa na rangi ya kijani. Nilibofya kitufe cha rangi ya kijani kisha nikarudi nyuma hatua tatu. Kabati lilichomoka mahali lilipo likawa kama linalonifuata lilipobakisha hatua moja kunifikia likasimama nikapiga hatua za kuhesabia kupitia upande wa kulia kama nitakaye kulizunguka, nikapita kwenye uwazi mdogo kwa nyuma kisha nikakutana na mlango kabla sijaingia kwenye ule mlango nilibofya tena kitufe cha kijani kabati likarudi mahala pake nikamaliza na kitufe chekundu ule mlango ukajifunga na kujiloki kabisa. Nilikuwa upande mwingine wa korido nyembamba iliyokuwa ina ngazi nyingi zilizokuwa zikielekea chini. Nilizifuata kisha nikapokelewa na eneo pana nikaziacha zile ngazi na kuingia kwenye mlango mwingine ambao haukuwa umefungwa. Macho yangu yakakutana na eneo kubwa lililokaliwa na gari tatu nyekundu mbili na moja nyeusi. Hizi zilikuwa maalumu kwa kazi ya humu humu ndani. Niliingia kwenye gari nyekundu ambayo ilikuwa iko tayari kuendeshwa na mimi kwani kila kitu cha kuniruhusu kuitumia kilikuwepo. Niliiwasha na kuigeuza na kupotelea kwenye barabara ya chini ya ardhi.




Dakika tano mbele nilikuwa kwenye ofisi muhimu na ya siri sana inayotambuliwa na watu muhimu wa kitengo hiki tofauti na wafanyakazi wengine. Mbele yangu alikuwapo mkuu wangu wa kazi mwalimu Daniel Matia Okale akiwa amekaa kimya akiitazama tarakilishi iliyoko mbele yake mithili asomaye taarifa fulani iliyomtaka utulivu. Nikapiga hatua mbili mbele nikiwa kwenye ukakamavu na kutoa salamu ya heshima ya kijeshi. Nilimsalimia kijeshi namna hiyo kisha nikafuata kiti kilichopo mbele yake nikaketi. Mwalimu Dao alinyanyua macho yake yaliyoonesha hali ya sinto fahamu kunitazama.




"Dokta Gabriel Nyagile ameuawa usiku wa kuamkia leo nyumbani kwake bila shaka taarifa hizi umezipata!" Alisema mwalimu Dao akinitazama vile vile. Nilinyong'onyea mikono, miguu, kiuno na kope zangu zikakosa utulivu zikabaki kupepesa kama natabana zongo.




"Mwalimu....! Dokta Gabi atakufaje....? Kwani ananini kilichopelekea kifo chake?" Nilimuuliza nikiwa hoi kiakili.




"Nilikuwa hapa nikitafakari muda wote huku nikitafuta majibu ya ni kwanini kama unavyoniuliza wewe sasa, jibu nililolipata kupitia fikra zangu ni kwamba huu haukuwa mpango wa kipumbavu, huu ulikuwa ni mpango kabambe na waliyowateka madaktari hawa na kuwapoteza walijua kuwa ipo siku kutatokea watu wa kweli na kuamua kulifuatilia hili hivyo wakaweka watu ambao pengine wapo kwa ajili ya kuzuia hili tu na si kitu kingine. Kuna uwezekano ulionekana wakati ukiwa unaingia kwenye ofisi ya Dokta Gabi kama si wewe basi ni vijana kutoka usalama wa taifa."




"Unataka kuniambia maafisa usalama wa taifa wapo kwenye njia ninazopita mimi?" Nikauliza kwa wahaka mkubwa.




"Hadi mtu anaaminiwa na kupewa kazi hii usitegemee akawa ni mtu mjinga lazima atakuwa mtu makini na mwenye kujua akifanyacho ili amiinike zaidi kwenye kazi yake. Siri kubwa ya mtu kupewa kazi ya kupeleleza hasa kwenye kitengo cha usalama wa taifa ni kufanya kazi kwa uhakika na kazi hiyo kuwa na mafanikio." Akanijibu mwalimu Dao, akili yangu ikabidi niipe kazi ya kurudisha matukio nyuma hivyo nikarudi hadi kwenye nyumba ya Dokta Omary Maboli Siki, nikaiona vile ilivyokuwa imechakuliwa vya kutosha sana nikajua hapa ndipo walipopata vielelezo vya kuwapeleka au kuwafikisha kwa Dokta Gabriel Nyagile.




Hata huyu muuaji pengine aliwaona hawa wanausalama kama siyo kuniona mimi....! Nini dhamira ya kuuwa kwake? Nikajiuliza akilini.




Lazima awe ameuawa kwa ajili ya kitu fulani kama siyo kunivuta mimi basi kuwavuta maafisa usalama wa taifa waliyomhoji marehemu nyuma yangu labda. Niliwaza bado huku nikijaribu kwa namna moja ama nyingine kujenga matukio.




"Wacha niende nyumbani kwa marehemu mkuu." Niliomba ruhusa kwa hili kwani nilikuwa na kila ushahidi wa kumpata muuaji akilini mwangu.




"Kwanini umepata wazo la kwenda huko?" Aliniuliza mwalimu Dao akinitazama usoni.




"Lazima muuaji alilenga kitu fulani na anataka kumvuta mtu aliyemuhoji marehemu, sasa huoni hapa nitaweza kumjua muuaji na kumshughulikia na huyu ndiye angenipa mwanga wa kujua ni wapi madaktari wetu wamepelekwa?" Nilimjibu nikiwa na hasira na chuki kwa mtu aliyesababisha kifo cha mzee yule mcheshi na mkarimu ambaye aliutoa muda wake na kunipa mimi tukasikilizana na kunipa majibu niyatakayo.




"Dhamira yako ni nzuri hata hivyo muuaji wa Dokta Nyagile hatapatikana kizembe kama anasavyo Mbu kwenye Chandarua chenye dawa kama unavyodhani na badala yake mtajazana wapelelezi kibao sehemu moja, ushahidi upo na unaonesha ni wapi madaktari wetu wamepelekwa kama mtu makini lazima utumie akili ya mwisho na hii ndiyo pekee inayotutofautisha sisi na wanausalama wengine. Sisi tunakuwa wa kwanza kulivamia tukio kabla ya wengine. Najua kuwa kinachokupeleka kwenye tukio la mauaji ni uchungu na chuki dhidi ya muuaji. Kimeniuma hata mimi kwa kuwa Dokta Gabriel Nyagile alikuwa ni suhuba wangu mkubwa wa siku nyingi, tufanye kazi kwanza tusisumbuane na muuaji ambaye ukichunguza kwa umakini utagundua kuwa nia na lengo lake ni moja. Safari ni kwenda Ungamo kama nilivyowahi kukuambia mwanzo na kama maelezo uliyopewa hayati Dokta Gabriel kupitia karatasi iliyoachwa na Dokta Lumoso. Nenda ukawalete madaktari wetu, nenda ukawarudishe wajuzi wetu na kama wamekufa tuko radhi kubeba makaburi yao na kuja kuwahifadhi nyumbani kwao kwa heshima zote. Nenda ukiwa na baraka zote kutoka kwa mkuu wa nchi, muheshimiwa Rais anaimani kubwa sana nasi anatuamini na kututegemea. Ukitoka hapa angalia kama unaakiba ya kutosha kwenye akaunti yako ya kazi kama huna usiwaze serikali imewekeza pesa nyingi kwa ajili ya kuirahisisha kazi yako. Ingia ofisini kwa Amiri akukabidhi pasi zako za kusafiria na vinginevyo. Usafiri wa kukutoa hapa hadi Dar es salaam upo Kilakala kwenye kiwanja cha mpira wa piguu wa vijana wa mtaa ule. Ni kama unaenda kilakala juu, ni Chopa ndogo ya jeshi iendayo kasi natumai hadi usiku wa leo utakuwa Ungamo kwenye nchi ndogo ya Afrika inayosumbuliwa na migogoro ya kisiasa." Akamaliza kuongea na kutoa maelekezo mwalimu Dao nami sikuwa na la zaidi nilitakiwa kuondoka kwani kila kitu kwa ajili ya safari nilikuwa nimekwisha beba. Nilitakiwa kuwa na paspoti kama tatu za kusafiria maalumu kwa ajili ya kazi yangu ambazo ningezikuta kwa Amiri. Vitu vingine muhimu na vya kughushi nilibeba huku nikiwa sijasahau silaha zangu za siri na za dhahiri. Nikasimama.




"Chukua hiyo bahasha inamaelekezo muhimu ukishafika Ungamo. Ukishaisoma karatasi iliyo ndani ya bahasha hiyo irudishe bahashani kisha utaikabidhi kwa mtu huyo ambaye jina lake utalikuta kwenye maelezo humo bahashani." Aliniambia mwalimu Dao baada ya kuniona nimesimama. Sikuwa na neno zaidi ya kuagana na mkuu wangu wa kazi nikapiga hatua hadi kuufikia mlango ambao ungenitoa hadi kwa katibu muhtasi anayefahamika kwa jina la Zuhura.




"Catherine!" Aliniita mkuu. Nikageuka kumtazama.




"Roi anakupenda sana hivyo ni vema ukarudi ukiwa hai." Sikumjibu kitu nilibakia nikitabasamu huku nikiufungua mlango na kutoka. Utani ni sehemu ya maisha yetu hivyo sikuwa na namna ya kumjibu. Nilifika kwa Zuhura nikamsalimia kwa bashasha kubwa naye akafurahi kuniona kwani ni kitambo kingi tulikuwa hatujaonana. Nilipoteza dakika kadhaa tukiongea hili na lile. Sikuwa na muda wa kupoteza sana niliingia kwenye chumba cha lifti nikaiamuru lifti hiyo inipeleke hadi ghorofa ya juu ambayo ilikuwa usawa wa ardhi kisha nikaingia kwenye chumba kimoja baada ya kutoka kwenye chumba cha lifti na kupita korido hii na ile. Nilimkuta Amiri akiwa na Chals wakipiga soga kwenye ofisi moja tulivu.




"Habari zenu jamani?" Niliwasabahi.




"Ooh! Shemeji letu hilo umekuwa adimu kama gurudumu za Meli. Kwanini hatuonani?" Aliuliza Chals.




"Ni mtihani wa maisha jamani kazi imekuwa ni sehemu kubwa ya kutufanya tusionane nadhani mnajua tulivyo na majukumu yasiyokwisha." Nilijibu huku nikiwa nimesimama wima.




"Najua umekuja kuhakiki barua yako ya kuomba likizo kama imefanyiwa kazi, huu ni wakati wako."




"Likizo ipo mnadhani, hakuna cha likizo wala nini hapa naelekea Dar es salaam kisha nje ya nchi." Nilijibu huku nikilieleke friji moja mule ofisini na kuchukua kinywaji laini na kukigida chote.




"Kazi....!"




"Unaongea vidogo tena, hivi nimekuja unipe vifaa vya kazi Chals kwani sina muda wa kupoteza kabisa kwanza acheni kunizingua kila kitu kiko wazi na mnajua. Amiri anajua na anamzigo wangu anatakiwa anipe." Alitaka kuongea Chals nikamkatisha akabaki kuachama kinywa chake.




"Kamata mkoba huo hapo uko na zana makini na zimepangiliwa vema" akasema Chals huku akitabasamu, nikashangaa. Walikuwa wanajua kila kitu ila waliamua kunizunguuka kwa kunitania nahisi furaha yao ni kuwa sijapewa likizo.


Wanabahati sana wangenitafuta kwa tochi.




SAFARI IMEUMA.








"Kamata mkoba huo hapo uko na zana makini na zimepangiliwa vema" akasema Chals huku akitabasamu, nikashangaa. Walikuwa wanajua kila kitu ila waliamua kunizunguuka kwa kunitania nahisi furaha yao ni kuwa sijapewa likizo.


Wanabahati sana wangenitafuta kwa tochi.




"Ndege ya kukutoa hapa nchini na kwenda kukutelekeza nchini Ungamo itaondoka tano asubuhi hivyo kwa mujibu wa saa yangu ni kwamba umebakiwa na saa mbili tu za kujidai bibie." Alisema Amiri pia, nikashangaa zaidi ingawa sikutia neno zaidi ya kumtazama.




Wapuuzi sana hawa. Niliwaza kisha Amiri akanikabidhi pasi zangu mbili za kughushi za kusafiria zenye majina tofauti ambayo ningeweza kuyatumia ingawa sikuona kama kuna umuhimu wowote wa kufanya hivyo hata hivyo ilinibidi kuvichukua kwa mkakati wa kazi yangu maana tahadhari ni bora kuliko kupambana na tatizo.




"Kila kitu kiko kwenye uwazi unaotambulika, hivyo Chals alikuwa akikudhihaki tu kuhusiana na likizo. Tuko tunakuchunga nyuma yako. Tunajua huendi kupambana na mtu mmoja huko uwendako na siku zote hakuna kazi ya kijasusi nyepesi. Tunahatarisha roho zetu kwenye kazi hizo ila ni matumaini yetu utafanikisha, kama mambo yakiwa magumu msaada utakujia hukohuko." Aliongea Amiri huku akiachana na tarakilishi na kunitazama usoni akiwa amesahau kulificha tabasamu lake kenye ushawishi mkubwa kwa mrembo yeyote yule.




"Naogopa kwa kuwa uko mwenyewe, sijui ni kwanini mkuu hakuniweka na mimi ili nikailinde mali ya kaka!" Akatania Amiri huku akinitazama kwa macho yenye mahaba mazito. Nilitabasamu na mwishowe kucheka kabisa kwa utani wa hao watu.




"Nimetengeneza mtambo wa kumfuatilia hukohuko aliko sasa ole wake ajisahau," Chals naye akachomekea. Niliwatazama kwa awamu tofauti huku nikiwa natabasamu.




Mngenipa matukio ya uchunguzi wa safari za kaka yenu ili nijue kafanya mangapi ya kunisaliti kwani mnadhani siijui tabia yake ya kupenda totoz, namstahi tu kwa kuwa sina ujanja kwake ila ningemfunga kamba ndani asitoke...!"




"Ungemfunga au mngemfunga..?"




"Umeanza Amiri...! Hivi ni muda gani utakua wewe? Muone kwanza...hebu nipisheni miye...!" Niliwaambia huku nikinyakua kilichosalia mezani kwao ambacho kilinihusu na kuufuata mlango wa kunitoa nje ya kile chumba huku nikiviweka vitu vyote kwenye begi dogo la kusafiria la kuvaa mgongoni. Nilijua walikuwa wakinisindikiza kwa macho nyuma yangu hivyo nikageuka nikiweka tabasamu usoni mwangu nikawafumania wakiwa wamekodoa macho wakinitazama, niliwakonyeza huku nikipotelea nje.




Nilirudi kwa njia ileile hadi pale nilipoegesha gari yangu nikaichukua na kutoka hadi barabarani. Nilipofika kituo cha daladala nikakunja kulia kwa mwendo kasi japo si wa kutisha. Nilipofika kwenye mzunguko wa NBC Bank sikuifuta barabara ya Old Dar es salaam niliingia kama nielekeaye kituo kikubwa cha polisi au kwenye uwanja wa Jamhuri Morogoro nikaipita mahakamani kwa mwendo wa kawaida sana, nilipofika mbele nikaingia kushoto na kuifuata barabara ya Morogoro Sekondari. Nikaupita ukumbi wa polisi kisha kuivuka barabara iliyokuwa ikienda chuo cha ufundi stadi Veta ikitokea Hospitali ya mkoa. Nikaendelea kuifuata barabara ya changarawe hadi nikipoupita uwanja wa mpira wa miguu uliopo nyuma ya jengo la kuhifadhia maiti la Hospitali ya mkoa wa Morogoro kisha kuliacha duka linalohusika na uuzaji na utengezaji wa masanduku ya kuzikia au kubebea maiti. Nikaenda mbele kidogo ambapo niliivuka barabara ya lami nikaingia shule ya msingi kisha kuvuka tena barabara ya lami iliyokuwa ikielekea Forest na kukipita chuo cha Ardhi kisha nyumba za polisi, mbele baada ya mwendo mfupi nikaingia kushoto na kuja kutokea Madizini. Punde nikawa Shule ya Sekondari ya wanawake ya Kilakala nikaifuata barabara moja kwa moja hadi nilipoina Helkopta husika mbele ya macho yangu hapo ndipo nilipo punguza mwendo nikasimama kabisa pembezoni mwa uwanja huo nikateremka. Nilipokuwa nikipiga hatua za haraka kuifuata Helkopta hiyo, rubani aliiwasha na kulifanya panga la Helkopta ile kuanza kuzungukua kwa kasi na kusababisha upepo mkali kuzunguka eneo hilo nikaingia na safari ikaanza.




_________




SEMBUYAGI, MABULE PAMOJA NA JACKOSON, hakuna kitu walichoambua kwenye uchunguzi wao kule kwenye nyumba ya hayati Dokta Gabriel Nyagile maeneo ya Mji mwema. Walijaribu kuangaza macho yao huku na kule huku wakijaribu kudodosa hiki na kile angalau kupata japo kitu hata hivyo kila kitu kilikuwa ni kwamba hakuna aliyejua muhusika wa mauaji hayo ni nani na kwa nini ameuwa. Maelezo yalikuwa yakijirudia yale yale kuwa Dokta Gabriel alipigwa risasi moja ya kifua upande wa kushoto ambayo ndiyo iliyosababisha mauti yake. Sembuyagi akajaribu kuwakabili askari polisi na kuwauliza mawili matatu baada ya kujitambulisha mbele ya askari hao kuwa yeye alikuwa ni afisa usalama wa taifa na akajaribu kutumbukiza hila zilizoendana na ukweli ili apate kitu bila askari hao kuhoji sana hata hivyo hao askari walikuwa na majibu yaleyale kuwa kilichomuuwa Daktari huyo ni risasi ambayo iliuchimba moyo wake vibaya sana huku jitihada za kumpata muuaji zikigonga mwamba. Wakaondoka wakiamini hawawezi kupata kitu na hawakuona sababu ya kuchelewa ikiwa walikuwa na jambo gumu la kumjua mtu anayejiita Musa. Wakarudi Dar es salaam. Kuwasilisha uchunguzi wao na baada ya hapo wakisubiri kazi nyingine ya kuendelea.




________




Mlipuko mkali wa risasi unasikika katikati ya mji wa Muavengero kwenye soko kubwa la mjini hapo. Mlipuko ule unawaacha watu wakihaha huku wengine wakitafuta mahali pa kujificha lakini kwa umbali wa mita sitini na tano, kunaonekana gari moja Noah ya rangi ya maziwa ikiwa imechanguka kioo kikubwa cha mbele na kuliacha gari hilo kwa upande wa mbele kuwa wazi kwa sekunde hizo chache. Taharuki ile inawafanya watu waliyokaribu na eneo hilo kukimbia na kwenda mbali na eneo lile lililosikika mlipuko wa risasi hata hivyo kwa ulivyo utaratibu wa watu, wale wa mbali na eneo la tukio wakatoka huko mbali na kulivamia eneo la tukio kuona kunani garini au kuna madhira gani yaliyojitokeza. Hawa wakabwatuka kwa sauti kubwa kabisa kuwa kuna mtu alikuwa ameuawa garini mule. Ikawa tafarani dhafarani, kila mja akataka kuona aliyeuawa huku wakisahau kilichomuuwa mtu huyo wamuonaye mfu wakati huo ni risasi ndiyo iliyoyapokonya maisha yake tena ambayo baadhi yao mlipuko wake waliukimbia kwa hofu kuu. Alikuwa ni mtu mzima mwenye haiba njema mtu huyo aliyeshambuliwa kwa risasi akiwa amevaa suti ya rangi ya kijivu ndani ya koti lake la suti akitanguliwa na shati la rangi nyeupe hakuwa amevaa tai. Punde watu walijaa hadi eneo hilo likawa halitoshi kila mmoja akizungumza la kwake kuhusiana na tukio hilo. Mashuhuda wakiwa wanaendelea na ushuhudiaji wa tukio hilo, pikipiki kubwa XLR iliegeshwa kwa umbali wa kama mita mia moja kisha mtu aliyekuwa akiliendesha pikipiki hilo akashuka na kuliacha hapo akipiga hatua kulisogelea eneo la kituo.




Frank Matiale Bambi mpelelezi makini sana kutokea kwenye kitengo cha upelelezi cha siri cha ungamo USS. Kitengo aminiwa ambacho tangu kuanzishwa kwake kimekuwa ni tishio kwa wavamizi na waharibifu wa amani ya nchi hiyo ndogo. Kitengo hiki kilianzishwa ndani ya utawala wa Rais Mabandu, utenguzi wa kutengua kila kilichokuwa kibovu, kila sekta na vitengo mbalimbali ulifanyika kwa maamuzi magumu mara baada ya kumuondoa na kumuangamiza Rais aliyetaka kufanya mapinduzi kwa serikali iliyokuwa madarakani kipindi hicho mara baada ya kumaliza muda wake. Mapinduzi hayo aliyotaka kuyafanya hayakuwa yakiongozwa na utashi wake bali alikuwa akishinikizwa na mrusi aliyekuwa akifahamika kwa jina la Chalcovich ambaye alitumia uwezo wake wa kifedha kutaka nchi hiyo ikamatwe na Mobande Julio Mobande ili alipe kisasi kwa aliyekuwa waziri mkuu wa nchi hiyo zamani kabla ya kuwa Rais wa sasa Muheshimiwa Backa Ramson Backa. Frank Matiale Bambi alipata mafunzo yake ya kijeshi na kijasusi kwenye nchi kadhaa hapa duniani kabla ya kurudi nchini kwake na kuingizwa moja kwa moja kazini hata hivyo kazi hiyo aliyotakiwa kuifanya ilikuwa bado mbichi na ni tishio kwa nchi. Ni kama mambo yale yaliyowahi kuikumba nchi hiyo kisiasa yalikuwa yakiendelea ndani ya kazi hiyo. Frank Matiale aliona jinsi ugumu utakavyoendelea kuwepo. Alikuwa na siku kadhaa tangu kukabidhiwa kazi hiyo na mkuu wake wa kazi bwana Gumzo Fataki, akimtaka afanye uchunguzi wa siri sana dhidi ya mauaji ya viongozi, wanausalama na baadhi ya raia ili ijulikane ni nani aliye nyuma ya mpango huo ili fagio la kusafisha limpitie na kuacha nchi katika hali ya usafi. Frank hakupata pa kuanzia japo kila uchao na uchwao alikuwa akichakalika alimradi ajue nini kingeweza kuwa mwanzo wa yeye kuingia kwenye jukumu lake. Mlipuko wa risasi uliotokea kwenye Soko kuu mjini hapo ulimvuta, hakuwa mbali sana na tukio, wakati mlipuko huo ukisikika yeye alikuwa kwenye Saluni moja kubwa na maarufu ya mjini hapo iliyofahamika kwa jina la Smart Berbashop. Hivyo watu walipohamanika na kuchoropoka kukimbilia kuliposikika tukio yeye akatumia fursa hiyo kubadili muonekano wake baada ya kulifungua begi lake la kubeba mgongoni akatoa koti la Kodrai la rangi ya ugoro akalitinga kisha akatoa na kofia ya chepeo akaitinga kisha akalitupia begi lake mgongoni na kutoka mule ndani ya ile Saluni akiwa kwenye muonekano mpya tofauti na alioingia nao saluni hapo akalielekea pikipiki lake na kuchukua uelekeo wa mahali uliposikika mlipuko wa risasi.




Frank Matiale Bambi aliutazama ule mkusanyiko uliyokuwa umelizunguka lile gari ambalo shoo yote ya mbele ilikuwa haitamaniki kwa kumwagwa kwa kioo chake baada ya risasi yenye nguvu kupenya, kichwani mwake alikuwa na mengi ya kujiuliza kuhusiana na tukio hilo shtukizi ambalo hakuwahi kulifikiria japo matukio ya risasi yalikuwa ni sehemu moja wapo ya burudani ya kukera masikioni mwa watu iliyokuwa ikirindima kila wakati hapo nyuma. Hali hiyo ilikwishaanza kusahaulika na watu wakaanza kuyarudi maisha yale waliyowahi kuyaishi hapo awali. Usahaulifu wa hali ya hatari kama ambayo imetokea hapo haikuwa na maana kuwa taifa lilikuwa limepoa moja kwa moja lah! Kulikuwa na fukuto baya la kisiasa lililokuwa likiichachafya serikali kupita maelezo, uchchafyaji huo ulikuwa ukiisumbua serikali ya Ungamo na Rais wake ndani kwa ndani kiasi kwamba huko kwenye makazi yao kukawa hakukaliki japo walijaribu kuumia wenyewe ili kuwaaminisha wananchi kwamba amani imerejea na Rais wao mpendwa Ramson Backa alikuwa akipigana kuhakikisha wanaishi kwa kujiaminisha kwamba hakukuwa na jambo lolote baya lenye kuhatarisha amani yao ya nchi. Hili lililokuwa limesahaulika karibu miaka mitano ama sita, linatukia punde tu tena kwenye kadamnasi ya watu. Hatua zake zinahesabika hadi alipolikaribia eneo la tukio. Kwanza kabisa kabla ya kufanya jambo lolote lile, Frank Matiale alichokifanya ni kuhakikisha eneo lile linajaa ndani ya ufahamu wake wa ubongo, analikagua lote na kujihakikishia kuwa hakuna kiumbe atakayemtilia shaka na akawepo kumchunguza. Muda mfupi baadae, Frank Matiale alishajihakikishia usalama na sura za watu wote wa eneo hilo alishazitupia kwenye retina yake ya jicho iliyotanguliwa na mboni imara inayoona kwa uangavu wa kutosheleza uliyokwenda kidato japo mboni hizo zilikuwa nyuma ya miwani ya jua ambayo kwa mtu asiye muelewa angeuumba muonekano wake huo kuwa ni wa kileo kwa kijana huyo. Watu walikuwa ni wengi na alitaka kupita kwenda kukagua huku akihitaji kwenda na muda ili kabla askari hawajalivamia eneo hilo awe ameshapata kitu cha kumsaidia katika uchunguzi wake. Frank Matiale alipita kwa haraka akiwapanguwa wale watu hadi alipokuwa mbele ya ile gari. Hakupoteza wakati aligeuka na kutazama tena watu kwa udadisi kisha akafungua mlango upande ule wa dereva akauacha wazi akimtazama muhanga wa risasi iliyopigwa kwa lengo stahiki la kuondoka na uhai wake.








Watu walikuwa ni wengi na alitaka kupita kwenda kukagua huku akihitaji kwenda na muda ili kabla askari hawajalivamia eneo hilo awe ameshapata kitu cha kumsaidia katika uchunguzi wake. Frank Matiale alipita kwa haraka akiwapanguwa wale watu hadi alipokuwa mbele ya ile gari. Hakupoteza wakati aligeuka na kutazama tena watu kwa udadisi kisha akafungua mlango upande ule wa dereva akauacha wazi akimtazama muhanga wa risasi iliyopigwa kwa lengo stahiki la kuondoka na uhai wake. Risasi hiyo ilichimba kifuani upande wa kushoto, damu nyingi zilikuwa zikimtoka upande wa mgongoni hiyo ikamuaminisha nguvu ya silaha iliyotumika haikuwa ndogo. Ilikuwa ni salaha iliyoshiba hasa au mpigaji huwenda hakuwa mbali na eneo hili. Akatazama kwa mbele ili kuweza kujiridhisha kama angeweza kuona mahali ambako mpigaji huyo alikaa, aliona uwazi kwa mbele hakukuwa na jengo lolote refu ambalo angeweza labda kuhisi aliyefanya hivyo ni mdunguaji. Akamtazama mtu huyo kwa sura kama angemfahamu au vyovyote. Hakumfahamu kwa haraka kiasi hicho, akajaribu kumpekua hapa na pale kupitia mifuko yake ya suruali hakuna kitu kingine zaidi ya simu moja ya kisasa na kibunda kidogo cha pesa. Akazirudisha zile pesa mahali alipozitoa kisha akahamia kwenye mifuko ya koti lake la suti kwa nje alikuta kitambulisho cha kazi hata hivyo mifuko ya ndani ya koti hilo hakukuta kitu cha aina yoyote. Akachukua ile simu akaitazama kwa muda kisha akairudisha mfukoni mwake baada ya kuona hakukuwa na simu yoyote iliyopigwa asubuhi hiyo wala ujumbe wowote. Akakigeuzageuza kile kitambulisho na kukisoma huku akijaribu kukariri jina na baadhi ya vitu. Alimtambua kupitia kile kitambulisho kuwa aliitwa Mansuli Bingwa jina hili likampelekea kukumbuka kuwa huyo alikuwa ni mkuu wa kituo cha polisi cha kati. Hii ilimtatiza kidogo kila alipojaribu kujiuliza kwanini mkuu huyo wa kituo cha polisi cha kati aliuawa. Akajaribu 'kucheki' hapa na pale akafungua hiki na kile kwenye dashi bodi ya gari ile akapata kuona bastola ndogo na fupi aina ya 2MM Kalibri zao maridhawa lililobuniwa huko nchini Austria. Aliichukua kwa tahadhari ya kutokuacha alama nyuma yake na kuitazama kisha akairejesha mahala pake. Akatazama kwenye viti vya nyuma Akaona mfuko mkubwa ambao ulikuwa umejaa mazagazaga mengi ya kula kama Machungwa, Mapeasi, Ndizi mbivu na mbichi, vipande kadhaa vya miwa na Ma-Apple. Pia kwenye mfuko mwengine mkubwa mweusi wa plastiki kuliwa na mboga za majani kama Mchicha, Kabeji, Chainizi huku kukiwa na Nyanya, Nyanya chungu, vitunguu na kadha wa kadha.




Alikuwa anatoka kukusanya bidhaa kwa mahitaji ya nyumbani....! Kwanini wamemuua...? Akawaza Frank Matiale Bambi. Hakuridhishwa na uchunguzi wake huo hivyo akawa anazidi kupekuwa hapa na pale huku akiyapuuzia macho ya mashuhuda waliyokuwa wakimtazama kwa kumjengea hoja vichwani mwao. Mara akasikia ving'ora vya gari za polisi vikiwa vimechachamaa. Akashuka na kuufunga mlango wa gari ile akiwa ameuacha mwili ule kama alivyoukuta hakuna alichobeba. Akavua glovu za mikononi na kuzitupia kwenye mfuko wa koti lake la Kodrai akajichanganya kwenye umati wa watu huku wengine wakishindwa kumuelewa alikuwa ni mtu wa namna gani. Hata polisi walipofika kwenye gari yeye alikuwa ameshaondoka eneo lile kwa kutumia pikipiki lake. Polisi wale walipofika eneo la tukio waliuliza hili na lile kwa waliyowakuta hapo huku wengine wakifanya upekuzi kwenye gari ile ya muhanga.




Muda mfupi baadae Frank Matiale alikuwa kwenye makutano ya barabara ya Uhindini kisha kuingia kushoto akiiacha barabara ya Zumo. Alipofika mbele kidogo tena akaingia kulia akiifuata barabara ya vumbi. Alinyoosha akiifuata barabara hiyo hadi alipofika kwenye eneo moja la wazi hapa akaegesha pikipiki yake pembeni mwa barabara kisha akatulia kwa nukta kadhaa, alikuwa akiyazunguusha macho yake huku na huko akiwa juu ya pikipiki kisha akaiondoa pikipiki hiyo kwa mwendo wa taratibu hadi nje ya jengo moja tulivu sana akaegesha pikipiki yake kisha akapiga hatua za taratibu kuusogelea mlango alipoufikia akatumbukiza mkono mfukoni mwa suruali yake akatoka na ufunguo akaufungua mlango huo akaingia ndani. Giza zito lilimpokea, haukuwa ni muda wa kuweza kuliruhusu giza litawale ila nyumba hii madirisha yake yalikuwa ni ya vioo vya giza ambavyo mtu akiwa nje ni vigumu kuona ndani kwa urahisi pia kwenye madirisha hayo kulipachikwa mapazia mazito ya rangi moja ya kuvuti. Hakutaka kufungua madirisha hayo alichokifanya Frank Matiale ni kuwasha taa ya sebuleni hapo. Mwanga ukafanikiwa kulikumbatia giza na kulificha. Sebule ilikuwa ya kuvutia sana. Kulikuwa na seti ya Sofa za kisasa meza ya gharama ya kioo kizito ambayo ilinakshiwa kwa maua maua kwenye miguu yake minene yenye rangi ya pekee. Zulia safi la manyoya ya rangi nyeupe na nyekundu iliyoambatana na mawingumawingu ililifanya zulia hilo lizidi kuleta mvuto wa hali ya juu na kuifanya sebule hiyo kuwa kwenye ubora wa kileo. Juu ya ile meza hakukuwa na vitu vingi sana zaidi kulikuwa na chupa moja ya pombe iliyotelekezwa kwa makusudi au bahati mbaya pia kulikuwako na kitambaa cha marembo ambacho kilijaa kwenye nusu ya meza hiyo na kuleta muonekano wa aina yake. Mbele ya ile sebule ukiwa upande wa mlango upande wa kulia kulikuwa na friji kubwa na kushoto kulikuwa na rafu ya wastani iliyo na vitabu kiasi. Alilisogelea Sofa moja na kuketi kwa utaratibu huku akilitoa begi lake mgongoni akilitupia pembeni ya hilo Sofa. Kichwani alijivika tafakuri ya aina yake na kubwa ilikuwa ni mauaji ambayo yalitokea mjini kwenye soko kuu. Akafikiri namna alivyokawia kufika eneo la tukio na kushindwa kujua watendi wa mauaji yale wamepotelea wapi. Akafikiri jinsi kioo cha mbele cha gari ile kilivyochanguliwa kwa risasi akajiuliza kama ilikuwa ni risasi moja iliyofanya vile hadi kukifikia kifua cha muhanga ama la! Hata hivyo kilichosikika ni mlipuko mmoja tu wa risasi hii ilimtanabaishia kuwa kishindo kile ndicho kilisababisha mauti ya mtu aliyemfahamu kama Mansuli Bingwa kupitia kitambulisho alichokipata kutoka kwenye mfuko wa koti wa marehemu. Hii ilimaanisha kuwa risasi hiyo moja ndiyo iliyochangua kioo na vilevile kufupisha maisha ya Mansuli.




Kwanini wamuue...? Akajikuta akijinyuka swali ambalo alishajinyuka mara nyingi kichwani mwake na hakulipatia jibu. Hata hivyo akazidi kulitafakari swali hilo kwa marefu na mapana ili angalau apate mwanga.




"Inamaana nitashindwa kujua kwanini wamemuua?" Akajiuliza kwa sauti. Alijua kufanya upelelezi wa kifo cha askari polisi ni vigumu kwa kuwa wenyewe watanadi kuwa wamejidhatiti katika kulipeleleza hilo.




"Lazima kuwe na mpango, nipange mpango ambao moja kwa moja utaniingiza kwenye upelelezi au utafiti wa kifo hiki kisha nikishajua sababu ya kwanini huwenda ikawa rahisi kuifanya kazi yangu." Akazidi kujishauri. Akaachana na hilo na kujilaza kwenye 'vono' safi laini la sofa lake akiupa starehe mgongo wake. Kichwani alikuwa na mengi Frank Matiale na mengi hayo ni ya muda ambao tangu kupewa kazi yake bado yalikuwa ni ya muda pia. Kifo cha aliyekuwa waziri wa ulinzi na usalama wa nchi marehemu Julius Kinanda na aliyekuwa mwanasheria mkuu mwanamama shupavu aliyepigana kufa na kupona akimtafutia mawakili imara Rais wa sasa ambaye miaka mitano iliyokwisha kupita alikuwa ni Waziri mkuu aliyewahi kupitia misukosuko mingi. Mwanamama huyo alifahamika kwa jina la Anastazia Mazibo, wote hawa wakiuawa kwa awamu tofauti na vifo vyao vikiwa tata pia muuaji asijulikane. Pamoja na kwamba uchunguzi wa vifo vyao ulilegalega hata hivyo kimya kifupi cha amani kikapita. Akashangaa mara tu baada kuteuliwa kwake kuingia kwenye uchunguzi anakutana na kifo kibichi tena kikiwa cha mkuu wa kituo cha polisi cha kati. Frank Matiale alikuwa na kumbukumbu zote za misukosuko iliyowahi kumpata muheshimiwa waziri Backa Ramson Backa kabla ya kuwa Rais. Alikumbuka kila kitu kwa kuwa hata yeye alikuwa ndani ya mapambano hayo akipata msaada mkubwa kutoka nchi ya Tanzania ambao ni majirani zao. Wengi wakimfahamu kama Frank Kichaa. Hili hasa ndilo lililokuwa jukumu lake la kwanza tangu alipotoka mafunzoni miezi mitatu nyuma. Akakumbuka maagizo yote aliyopewa na mkuu wake wa kazi, akaikumbuka historia iliyoshiba ambayo mkuu wake alimpatia na mwisho kabisa akapewa jukumu la operesheni safisha akitakiwa ahakikishe wamiliki wa upuuzi huo uliokuwa ukiendelea na huo ulioibuka upya anawatia mikononi ama kuwafundisha adabu vile inavyowezekana hadi wampatie ukweli uliyoshiba ambao moja kwa moja utamuingiza mchezoni kuitengeneza historia mpya ya maisha ya amani. Akatabasamu kwa jinsi mchezo huu ulivyo wa kipee na ugumu alioupa na jinsi alivyotakiwa kuwa makini.




"Hakika ni mpango kabambe." Akajisemea tena huku macho yake yakizidi kuishangaa sebule yake ambayo ilikuwa ikimpa faraja kila aitazamapo. Aliipenda sana nyumba yake na alipenda kuwepo hapo muda wote apatapo nafasi ya kuuhitaji utulivu zaidi. Sasa aliona namna atakavyo ikumbuka kwa kuwa mbali nayo hadi pale kila kitu kitakapo kuwa sawa.




___________




SAA KUMI NA DAKIKA AROBAINI NA TATU ZA JIONI, NILIKUWA KATIKATI YA JIJI LA MUAVENGERO NIKIKATIZA HAPA NA PALE, HUKU NA KULE. Ni muda mfupi tangu nitoke uwanja wa ndege wa kimataifa wa Tao De. Macho yangu yalikuwa yakiushangaa mji huu ulivyo wa pekee, ulikuwa mtulivu kuliko majiji yote ambayo nilishawahi kuyatembea hapa Afrika ya mashariki na Afrika yote kwa ujumla wake. Wakazi wa mji huu walikuwa wachakalikaji kila niliyemuona au kupishana naye alikuwa kwenye mihangaiko yake hakuna ambaye alikaa kihasarahasara. Vijiwe vyote vilikuwa na watu hata hivyo hawakuwa wamekaa bure hapo ungekutana na kila aina ya mishughuliko, ungekutana na muuza Kahawa, ungekutana na fundi Baiskeli, ungekutana na wauza magazeti na pia usingeweza kukosa madalali hata kidogo kwenye vijiwe hivyo alimradi shughuli na watu na watu na shughuli.


Hawakukaa bure.




Nilikuwa natokea barabara ya K2 nikiivuka barabara moja ya watembea kwa miguu kisha nikataka kuvuka barabara nyingine iliyokuwa ikielekea kwenye msikiti mkuu wa mjini hapo. Nilisubiri kwanza magari mawili yanipite ndipo nivuke. Nilikuwa nimevaa suruali ya Jeans ya rangi nyeusi, kiatu cha ngozi, fulana ya mikono mirefu nzito iliyounganishwa na kofia ambayo nayo niliitupia mgongoni huku kofia ya kapelo ikiwa imenikaa kichwani barabara, miwani ya rangi nyeusi na mkononi nikiitupia saa yangu ile niipendayo. Sikuwa nikitembea kwa haraka sana, mwendo wangu ulikuwa wa wastani. Niliyavuka maduka kadhaa ya nguo na kuzipita saluni za kike kabla ya kukunja kona moja upande wa kulia ambako kulikuwa na mlolongo wa maduka mengi mchanganyiko. Nilizidi kujipa ugeni wa eneo hili kila nilipokuwa nikipita sikuacha kuyaendesha macho yangu katika kushangaa. Mbele yangu kulikuwa na duka kubwa la nguo za kike na za watoto mchanganyiko, kichwani mwangu kulikuwa kukipita mambo mengi sana, nilijaribu kuyapangilia angalau yawe kwenye mpangilio ulionyooka hata hivyo niliona mengi yakinichanganya. Nilitembea kama mtu lakini akili yangu ilifanya kazi mithili mtambo mkubwa unaosukumwa na Kompyuta. Nilikuwa nimebakisha hatua chache ili kuweza kulifikia lile duka kubwa la nguo. Sikuwa mbali nalo na nilipolifikia kabla sijalipita, masikio yangu yakaumizwa na mlipuko mkubwa wa risasi ambayo kwa mlipuko ule bila shaka ilisukumwa na mashine yenye nguvu. Sikusubiri ushuhuda unitokee na kunijuza hicho kilichotokea kilikuwa ni nini nilikuwa mzoefu wa purukushani hizo hivyo mapema sana nikawa nimejua nini kimetokea. Nikatuliza akili kisha nikaupa utulivu mwili macho yangu yakifanya kazi kwa umakini mkubwa. Nikaona watu wakikimbilia eneo ambalo mlipuko huo ulitokea, sikuwa na mizigo ya kunisumbua na kunifanya niwe mzito nilibeba begi langu dogo mgoni hivyo niliweza kufanya lolote na nisiwe kituko kwenye macho ya watu. Nilijichanganya na wale wanaokimbia kuliko na tukio. Kwa kuwa sikuchelewa kufika eneo la tukio haraka sana nilichokifanya ni kutazama nini kimetokea na ule umlipuko ulikuwa na maana gani. Nikaiona gari aina ya Noah rangi ya maziwa ikiwa imechanguliwa kioo kwa mbele hivyo haraka sana nikajua mtu au watu walioshambulia walikuwa upande ambao mimi niliupa mgongo, sikupoteza muda niligeuka nyuma kwa haraka sana nikaiona gari ndogo Toyota Vitara ikiondoka kwa kasi kubwa sana. Nilishtuka na kujikuta nikichoropoka na kuanza kuikimbiza kutokea hapo, nilikimbia kwa mwendo wa kutokutiliwa maanani na sikuwa nikiifuata kwa nyuma, nilipita katikati ya majengo mawili na kutokea upande wa pili huko nikaiona ile gari ikiingia barabarani na kuongeza kasi mara dufu. Haukuwa mwendo mdogo niliifuata kwa kujaribu kuongeza kasi yangu hata hivyo ilikuwa ni kama Kobe kumkimbiza Sungura.


Iliniachwa kwenye mataa.




Nilipunguza kasi nikiitazama gari ile ikitokomea mbali zaidi.




NI WAZI WAUAJI AMEWAONA SASA JE, WAUAJI NAO WAMEMUONA CATHERINE? VIPI KUHUSU FRANK MATIALE?








Nilishtuka na kujikuta nikichoropoka na kuanza kuikimbiza kutokea hapo, nilikimbia kwa mwendo wa kutokutiliwa maanani na sikuwa nikiifuata kwa nyuma, nilipita katikati ya majengo mawili na kutokea upande wa pili huko nikaiona ile gari ikiingia barabarani na kuongeza kasi mara dufu. Haukuwa mwendo mdogo niliifuata kwa kujaribu kuongeza kasi yangu hata hivyo ilikuwa ni kama Kobe kumkimbiza Sungura.


Iliniachwa kwenye mataa.




Nilipunguza kasi nikiitazama gari ile ikitokomea mbali zaidi. Niliikariri namba ya gari pamoja na jinsi ilivyo kisha nikaiacha inisolole kwa kuniacha kwenye mataa. Haraka sana nikalikumbuka lile tukio la kuharibiwa ile gari kwenye kioo chake cha mbele hivyo nilirudi nyuma haraka huku nikiungana na watu wengine waliokuwa bado wakikimbilia kwenye tukio hilo. Nilipofika nilikuta umati mkunwa wa watu ukiwa umeweka msitu mkubwa kiasi kunipelekea nishangae kidogo kwa jambo lile.




Hii kweli ni Afrika yetu niijuayo. Nilijiwazia baada ya kuona watu wengi kiasi kile. Picha nzima ya tukio ikanijia ghafula kichwani mwangu ikanipelekea kuuliza wale watu kwanini walimuua huyo mtu ambaye alikuwa hajitambui garini kwa wakati huo na watu wakalifanya ni tukio la kuvutia hata kujisogeza karibu zaidi. Jibu sikulipata kwa haraka ijapokuwa nilikuwa na uhakika hakukuwa na mtu mjinga mwenye kuamua upunguani wa kuyatoa maisha ya mtu pasi na sababu za msingi.




Lipo jambo. Nikajihakikishia. Pamoja na kuwaza ama kufikiria sana hata hivyo nilikuwa makini na kila kilichokuwa kikiendelea mahala hapo. Niliona mashuhuda wakipiga picha tukio hilo kwa kutumia simu zao za gharama ili baada ya muda wajizolee sifa mitandaoni kwa Coment na Like za kutosha kwa picha hiyo ambayo ilihuzunisha na kuogopesha kuitazama huku pengine wakienda kuinadi kwa kasi wakiipamba kwa maneno kama; watu hawana huruma, binadamu tumekosa utu, hivi sasa wanyama wanahuruma kuliko wanadamu, tukio la kuhuzunisha, watu wasiyojulikana wamefanya yao, mtu mmoja achapwa risasi na watu wasiyojulikana. Mengi na mengine kama hayo yatazipamba akaunti zao mitandaoni huku wakijivika huzuni. Wengine walikuwa wakisogea karibu kabisa na nilipowaangalia vizuri usoni hawakuwa wakionesha kama walikuwa na sura za uandishi wa habari hata wa kujitegemea.


Hawakuwa nao.




Niligeuza macho yangu huku na kule nikizidi kulichunguza eneo lile sikutaka kusogea eneo la tukio kwa ukaribu zaidi kwanza kuna kitu nilitaka kukiona kama kingeweza kutokea eneo hilo na kile ambacho kingefanyika. Nilitaka kuona ujaji wa askari polisi kwanza na muda ambao wangefika hata hivyo sikuona dalili za askari polisi wala sauti ya gari zao. Taratibu wazo la kusogea karibu na kufanya uchunguzi wangu likanijia hata hivyo muda mfupi wazo hilo nikalirudisha kwapani mara baada ya kumuona kijana mmoja akilisogelea lile gari akitokea kwenye pikipiki kubwa XLR ambalo aliliegesha umbali mdogo kutokea hapo. Alikuwa ameyaficha macho yake nyuma ya miwani myeusi, alivaa suruali ya Jeans ya buluu mpauko chini akiwa amevaa kiatu kizito cha ngozi cheusi halafu juu akamaliza na shati jepesi la rangi nyeupe sambamba na koti zito la Kodrai la rangi ya ugoro. Kijana huyu alinivutia kumtazama mara baada ya kumuona anavyotembea na jinsi anavyowapangua watu ili kujipatia njia, umakini aliyojivika na jinsi alivyokuwa akiigeuza mara kwa mara shingo yake kutazama kila upande wa eneo lile, nikajua hakuwa mtu wa kawaida. Hisia zangu ziliniambia hivyo ingawa sikupenda kujiridhisha bila kupata ushahidi thabiti.




"Si mtu wa kawaida huyu!" Nilijisemea mwenyewe kwa sauti ya mkono wa birika huku nikizidi kumtazama. Nilimuona akilikaribia lile gari aina ya Noah lenye rangi ya maziwa kisha akaufungua mlango wa upande wa dereva na kuyashuhudisha macho yake kwa upande wa ndani. Kabla hajapanda kwa kuukanyaga mguu wake kwenye eneo kama ngazi, aligeuza shingo yake kwa mtindo wa nusu duara na ni kwa haraka mno. Nikajihakikishia kuwa huyu hakuwa mtu wa kawaida kama nilivyodhani. Akaanza kumpekuwa yule marehemu hadi akaridhika. Punde nikaanza kusikia sauti za ving'ora vya gari za polisi. Yule kijana aliteremka kwenye ile gari kisha akaufunga mlango vile vile na kuondoka akiifuata pikipiki yake. Nikamfuatilia kwa macho huku nikijaribu kutaka kuuhifadhi muonekano wake kwenye ufahamu wa akili yangu. Aliondoka hilo eneo nami nikajiondoa huku nikiwa na imani kuwa huwenda hii ndiyo kazi iliyonileta kwenye hii nchi ambayo kihistoria bado ilikuwa na vuguvugu la vurugu za kisiasa lisilo poa.




Nilikuwa na nafasi kubwa sana ya kuweza kumfuatilia yule kijana ili nimjue kiundani lakini hata kama ningemfuatilia bado ingenilazimu niwe na hoja nzito ya kufanya hivyo, niwe na majibu ya maswali nitakayojiuliza mwenyewe ya kwanini namfuatilia...? Nilikuwa sijafika nilipotakiwa kufika na ilikuwa ni lazima nifike hapo ndipo nijue nafanya nini na naanzia wapi. Sikuona sababu ya kuendelea kuwepo hapo hata kidogo niliinyoosha miguu yangu initoe hilo eneo na kutafuta namna ya kufanya. Nikiwa napiga hatua za taratibu huku uso wangu nikiwa nimeuelekezea chini, akili yangu ikakumbuka maagizo niliyopewa na mkuu wangu wa kazi kuwa ni lazima nihakikishe sijihusishi na kitu au jambo lolote hadi nifike kwa mtu mmoja ambaye alifahamika kwa jina la Abdallah Khalid Mapande au AKM. Alinipa sifa za huyo mtu na uhodari wake lakini pia alikuwa ni mtu asiyependa kuishi na watu aghalabu alijitenga sana na kuishi mwenyewe. Aliwahi kuwa mwanajeshi wa miaka mingi ambaye hadi anaacha kazi ya jeshi alikuwa na cheo cha Luteni. Huyu mtu alikuwa ni muhimu sana na mpenda haki. Sifa zote hizo mwalimu Daniel Okale alimjaza mtu huyo na maelezo yake kuyaweka kwenye karatasi bahashani ambayo alitaka niisome. Nilikuwa na ulazima wa kufika kwake hivyo sikupaswa kupindisha.




Nilikuwa najua ni wapi hasa ningeweza kumpata huyo mtu hivyo sikuwa na shaka, hapo nilikuwa tayari nimekwisha chepuka kwenye kona kadhaa nikiwa naifuata barabara ndogo iliyojaa vurugu za watembeyao kwa miguu. Njia nzima simulizi zilikuwa ni za tukio lililotoke punde kwenye soko kuu. Ukimya wangu ukazidi kunipa kujua mengi kwani kila mtu aliongea lake huyu akisema kuwa huwenda yale waliyokuwa wameanza kuyasahau sasa yalikuwa yakijirudia tena.




"Hapana bwana hawa huwenda walikuwa na visasi vyao au majambazi wameamua kufanya yao maisha magumu sana sasa hivi, mimi siamini kama yaliyotokea nyuma yanaweza kurudi tena wacha tuishi na amani yetu bwana usiombe kile kitu kirejee." Mmoja wa watu hao alisema. Wengi walionekana kumpinga huyu aliyetoa hoja ya kwamba huwenda kile kilichotokea miaka mitano iliyopita labda kinaweza kujirudia, nilitabasamu moyoni kwani nilikuwa na uhakika kuwa kilichokuwa kikiwasumbua wengi ni woga na si kitu kingine. Ile hali ilitisha sana kwa kweli hata mimi sikutamani itokee bali ibaki tu historia kuwa kuliibuka angamizo moja lililotengenezwa na wapuuzi wachache lililotaka kuangamiza watu wengi Tanzania na Ungamo. Niliwafuata wale watembeyao kwa miguu hadi nilipokiona kituo cha mabasi madogo upande wangu wa kushoto mbele. Nikapiga hatua tatu mara baada ya kukunja upande huo kisha nikasubiri Roli kubwa la mchanga lipite nami nikaivuka barabara hiyo. Niliyapa macho yangu kazi ya kuangalia usafiri ambao ningeweza kuutumia hadi kwenye kijiji cha Asumile kilichopo Kilometa tano kutokea mjini hapo. Nilikuwa na ramani yangu ndogo ya kijasusi iliyoko kwenye karatasi ngumu mithili ya msasa ambayo ingeniwezesha kufika huko kwa wepesi zaidi pasipo kupata usumbufu wa aina yoyote. Pitapita yangu hapa na pale nikaona basi dogo aina ya Costa iliyochoka. Nyuma iliandikwa maneno ambayo ni kawaida kwa mabasi mengi au magari mengi kuandikwa. 'NAJUA KIFUA CHAKO HAKITUNZI SIRI, YA MKEO SIKWAMBII!' Hivyo ndivyo ilivyokuwa imeandikwa nyuma kwenye kioo kwa maandishi ya rangi nyekundu. Ilijaa vumbi mno na wahusika hawakuthubutu kulifuta wala kujaribu kushughulika na hilo. Kulikuwa na vijana wengi kwenye kibanda cha kupumzikia abiria wakiwa wanabishania mambo yao binafsi hakukuwa na zile purukushani za upigaji wa debe kama vituo vingi vya mabasi vilivyo. Nikajua kuwa hapa niko kwenye kituo halisi cha mabasi yaendayo safari za lazima yaani ukitaka utaenda hutaki acha. Watu wengi hususani vijana wakawa wakinitupia sana macho bila shaka ni kwa jinsi ambavyo nilivaa. Sikuwatilia shaka na sikutaka kujaji sana nini kilichomo kwenye fikra zao nilichokuwa nikifikiria ni namna ya kupata gari la kunifikisha niendako. Gari hili mbele liliandikwa Bantu, nikajua nimefika kwenye basi husika kwani ramani yangu ilikuwa ikiniambia kuwa kutokea hapo hadi Bantu ni zaidi ya kilometa zisizo pungua nane na hadi kufika huko unapita vijiji viwili kwanza ni Asumile kisha Ngena ndipo uingie Kijiji cha Bantu. Hivyo sikuwa na budi kuparamia gari hiyo. Niliunyanyua mkono wangu uliobeba saa nikatazama muda, muda ulikuwa ukienda sana na sikuwa na uhakika huwa wanatumia muda gani wakiwa barabarani hadi kufikia hapo kijijini Asumile. Gari ilikuwa imejaa, si kujaa kwa watu wake kukaa lah! Siti nyingi zilijaa mizigo kuashiria kuwa zimeshikiliwa na watu na huo ndiyo ulikuwa utaratibu wa hapo hata hivyo Mungu alinisaidia nikabahatisha siti ya dirishani nikakaa lakini ilihitaji moyo sana maana viti vyake vilijaa vumbi jekundu kupita maelezo.




"Huwezi kuchafuka dada usitishiwe na hilo vumbi kwenye kiti!" Sauti ya kijana mmoja ambaye alikuwa akisubiri mimi nikae ndipo naye atoe mzigo wake uliyokuwa ukishikilia kiti akae, iliniambia nilipokuwa nakikagua kile kiti baada ya kukaa. Nilitabasamu kirembo nikiwa namtazama usoni huku nikiweka haya za kike ingawa si zile za kumnyima urafiki.




"Hapana si kama nahofia vumbi ila ni mara yangu ya kwanza kupanda gari namna hii hivyo lazima nistaajabu." Niliongea kwa sauti yangu halisi ya kike hii sauti ndiyo ilikuwa silaha yangu kubwa sana Catherine. Nikikudhamiria huwa sikuachi salama. Ila sikupenda mazoea na watu walioonesha dalili ya kunitamani kwani nilimuheshimu sana mpenzi wangu na pia nilijiheshimu.




"Kwani ni mgeni wa njia hii?" Yule kijana akaniuliza swali ambalo nilishamjibu kama angetumia akili ya ziada asingehangaika kuniuliza swali la namna hii, sikuringa nilimjibu.




"Ni mara yangu ya kwanza kuipita njia hii."




"Unaonekana, sidhani kama pia ni mwenyeji wa huu mji maana sijawahi kukuona hapa mjini dada yangu?"




"Unataka kuniambia kuwa wote wanaoishi hapa mjini ni watu unao wafahamu?" Nilimuuliza huku lile tabasamu langu likizidi kunawiri usoni mwangu.




"Hapana si kama wengi nawajua ila hata muonekano wako si wa muda mrefu hapa maana watu wa hapa wanajulikana bwana," alizidi kulazimisha kwa kuing'ang'ania hoja yake. Nikafikiri kwa sekunde kadhaa nikaona haina haja ya kuendelea kumkatalia.




"Yaa, mimi si mwenyeji sana wa hapa japo huwa nafika mara nyingi ndani ya mji huu kwa ajili ya matembezi ya hapa na pale hasa nyakati za likizo hivyo nimekuja kimatembezi na nipo kwa majuma kadhaa."




"Nililijua hilo kuwa niko na binti msomi na mrembo hasa...vipi huku nako unakwenda kwa nani maana sidhani kama kuna usafiri wa kurudi nyuma tena leo, hii ni gari ya mwisho kutoka hapa mjini na kuna gari tutapishana nayo njiani nayo ni ya mwisho kutoka Bantu, una ndugu huku?" Akaniuliza yule kijana huku akionekana kuhitaji kunizoea zaidi. Hila za wanaume nilizijua hivyo sikuwa na shaka juu ya hilo. Nikiwa najiandaa kumjibu, gari iliwashwa kisha ikaungurumishwa kidogo na kupigwa 'maresi' moshi mwingi mweusi ulifumuka na kulimeza eneo kubwa la kituoni hapo, madirisha yalikuwa wazi hivyo moshi ule mweusi ukawa unaingia madirishani na kuleta kero ambayo ilinikera mimi tu huku wengine wakionekana kuizoea adha hiyo, sikuvumilia nilitoa kitambaa changu cha leso na kuziba pua na mdomo huku nikiyaacha macho yakichonotwa kwa machozi.




Huu moshi au bomu la machozi...? Nikajiuliza nafsini. Mayowe yalirindima huko nje kuashiria kuwa vijana wengi walikuwa wakivutiwa na kitendo hicho cha kukera.




"Kangafu' hiloo...., 'Jogoo la shamba'....., 'Ngongingoo!" Sauti za vijana zilihanikiza wakilipa majina hilo gari kwa sifa hata hivyo majina hayo yalionekana kuwa ni majina batizo yaliyokubaliwa na gari hilo kwani wakati majina hayo yakining'inizwa hewani kutokea kwenye vinywa vya vijana hao, gari ikawa inaitika kwa kuunguruma kama mabati yenye kutu yagonganavyo. Dereva wa gari hiyo naye akapewa bichwa la ziada akawa anazidisha kitendo kile cha kukera hata hivyo wengi walionekana kukizoea.




"Inabidi hii hali uizoee mrembo maana haya ndiyo maisha yetu...pole sana!" Yule kijana alionekana kunihurumia nami nikajiachia kabisa nikajifanya kujiinamia. Punde gari ikaondolewa na nikauhisi ukongwe wa chasesi ya gari hiyo kwani msuguano wa nyuma ulikuwa mkubwa sana kiasi sauti zenye kuleta kelele zikayaumiza masikio yangu nikataka nilidhibiti hilo kwa kufunga kioo angalau. Lahaula! Kioo kilikuwa kama kimeshikiliwa na gundi hakikusogea wala kujongea. Likanishuka, sura ikapwaya nikasema hewala! Nikamkabidhi Mungu roho yangu huku garini nikiacha mwili unaotambua yaendeleayo kwa kujitakia.




Ukitaka safari isiyokera tumia gari lako. Angalau kauli hiyo iliponijia kichwani, nikameza funda la mate na kumshukuru Mungu.


Safari ikaendelea.




"Kwahiyo huku unaenda kwa nani au una ndugu? Akaniuliza tena lile swali ambalo kwa akili yangu nilitaka kulipuuzia.


Huyu naye king'ang'anizi. Nikamteta.




"Aam, yaa, huku yupo rafiki yangu niliwahi kusoma naye chuo, maisha yakatuweka mbalimbali sasa ameniambia yuko nyumbani kwao likizo ndiyo nakwenda kumtembelea," nilimjibu vile alivyotaka kujibiwa kulikuwa hakuna namna nyingine zaidi ya kumridhisha kwa uwongo wenye kuendana na ukweli.




HUYU KIJANA SINA HAKIKA KAMA ATAKUWA NI MWEMA KWA CATHERINE SI KWA MASWALI HAYA.








"Aam, yaa, huku yupo rafiki yangu niliwahi kusoma naye chuo, maisha yakatuweka mbalimbali sasa ameniambia yuko nyumbani kwao likizo ndiyo nakwenda kumtembelea," nilimjibu vile alivyotaka kujibiwa kulikuwa hakuna namna nyingine zaidi ya kumridhisha kwa uwongo wenye kuendana na ukweli. Kimya kikapita bila kuuliza swali jingine, sauti ya vyuma vya gari kutoka kwenye baadhi ya maungio yake zikazidi kusikika kutokana na 'minemba' ya barabara hiyo chakavu. Sauti zile zikawa kama ala mbaya ya muziki nisiyotamani kuisikiliza maisha yangu yote. Nikamsikia huyo kijana akijikohoza nikajua muda wowote anaweza kuniuliza maana haishiwi maneno kama kunguru wa pwani, ikawa kama nilivyowaza.




"Unarudi kesho au?" Sikumjibu kwa haraka nilimtazama kwa tuo huku sasa nikililazimisha tabasamu, nikatia mkono kwenye mfuko wa ile fulana niliyovaa nikatoa PK na kuitia kinywani baada ya kuimenya, sikuwa mpenzi wa hivi vitu na si tabia yangu ila kuna wakati nalazimika kutumia na aghalabu sana huwa ni pale ninapomaliza kuvuta sigara au nikiwa nasafiri kwenye usafiri wa uma kama huu napenda kutafuna PK ili kujiweka katika utulivu wa kutohitaji usumbufu.




"Nitarudi kesho!" Nilimjibu kisha nikageukia dirishani hii ilimaanisha kuwa sikuhitaji usumbufu maana uchagizaji wake wa maswali ulishanichosha.


Hakuwa huyo kisebengo.




"Samahani, sijakufahamu jina lako mrembo sijui unaitwa nani?" Aliniuliza. Nikajifanya kiziwi ili tu asiendelee kunisumbua sana. Akarudia, huyu alikuwa king'ang'anizi nilichukia hata hivyo mara nikauhisi moyo wangu ukitabasamu, nilijikuta nikiihusudu ghafula tabia yake huku nikijishangaa na moyoni mwangu kuna wazo jipya kuhusu huyo kijana lilinijia na kuona linaweza kuwa na tija japo sikujua ni kwa wakati gani na kwa namna gani hivyo nilimtazama kwa jicho lililodhihirisha uchovu nilianza kutengeneza hila ili ajue kuwa nimechoka sana.




"Naitwa Jamila Mamboleo," sikuwa na budi kumdanganya na hilo halikuwa la kushangaza hasa kwa kazi yangu ya kijasusi, nilimjibu kivivuvivu nikijilaza kwenye kile kiti macho yangu yakiangaza nje, nikajua fika macho yake ya tamaa yalikuwa yakikitazama kifua changu kisha kuitazama shingo yangu ya upanga. Nilizisikia pumzi zake zikishuka kwa nguvu nikajua koo limeshaanza kumuwasha ila hakuwa na kitu anachoweza kuniuliza. Nikageuka kivivu huku jicho nikiliweka katika uchovu uleule ambao kwa asilimia kubwa ulikuwa ukizisumbua na kuzitongoza hisia zake za kishenzi.


Jicho langu lilikuwa fimbo nalo.




"Hutaki nikujue kwa kuwa umeridhika na ulichokipata...? Wanaume nawaogopa hapo tu, haya endelea kukaa kimya kwa kuwa umepata ulichokitaka," nilimuwahi kumuuliza kwa kumchokoza.




"Aaah! Hapana dada nimeona jinsi ulivyo choka nikakosa namna...mimi naitwa Jamali Maigwa ni mwenyeji wa mji huu wa Muavengero nimezaliwa na kukulia mtaa wa Uhindini. Ni mtu maarufu sana popote mjini hapa ukiuliza tu JM umenipata, maskani yangu hasa ni mtoni huko ndiko nilikosimika kibanda changu. Huku kuna mzigo wangu nakwenda kuukagua kama umeshakamilika pia kuna pesa ya kuongezea nakwenda kuwapa wakusanyaji si unajua tena mjini mipango dada yangu?" Akamaliza kujikanyaga, alimaliza kila kitu nikaamua kumuacha maana kama ningeamua kumuuliza swali jingine huwenda angenielezea hadi utamu wa mkewe kama ameshaoa.




"Nimefurahi sana kumpata mwenyeji wa Muavengero maana najua utanitembeza sehemu nyingi nikihitaji msaada huo." Nilimwambia huku nikijiweka vizuri zaidi na kuitupia kofia yangu ya Prova kichwani nikaomba utulivu huku nikijua fika nimemchokoza na ile dhamira yangu ilikuwa bado inachemka moyoni mwangu.




___________




Gari ilinung'unika ikalia na kucheka kicheko cha maumivu huku vumbi jekundu likinyanyuka nyuma baada ya gari hiyo kupita na kusambaa hewani kwa shangwe kubwa kisha kutuama pembezoni mwa barabara hiyo ya vumbi na kuyafanya majani yake kupoteza ukijani na kukumbatiwa na rangi isiyoeleweka kama ni nyeusi au kijivu. Majani mengi yalikufa kwa mtindo huu. Mwendo ulikuwa mrefu na wa kuchosha hata hivyo haikuwa na maana kuwa tusingefika mwisho wa safari. Saa yangu iliniambia kuwa muda ulikuwa si rafiki kwangu kabisa na ulikuwa ukizidi kuyoyoma.




"Haya wale wanaoshuka Asumile wajisogeze mbele!" Sauti ya utingo iliniweka sawa na kujikalisha vizuri kitini nikamuomba Jamali Maigwa anipishe nipite maana mimi nilikuwa nimeshafika mwisho wa safari yangu.




"Umefika mwisho?" Aliniuliza Jamali akionesha kutokuamini.




"Ndiyo, mimi naishia hapa rafiki," nilimjibu huku nikimuachia kadi maalumu ambayo ilibeba namba zangu za simu. Sikutaka kumuacha hivihivi kwani kila nikimtazama kuna kitu nilikuwa nikikiona moyoni mwangu sijui hata ni nini labda ni vile tu alivyoniambia yeye ni mwenyeji wa mji huo.




"Ningependa tuwasiliane kama huto jali," nilimwambia nikiwa nimekwisha kumpita, najua nilimuacha na kigagaizo asiamini kama nimeweza kumpa namba zangu za simu sikujali nilizidi kupita mbele nilibanana na watu hadi nilipofika mbele karibu na alipo kondakta wa gari hiyo.




"Dada unashuka hapa eenh?" Aliniuliza kondakta wa gari hiyo ambaye kwa mtazamo aliendana na gari yenyewe, alikuwa mchafu sana wa mavazi. Nikamjibu kwa kutikisa kichwa changu juu chini.




"Fungua pochi kabisa tunakimbizana na muda dada," alisema. Sikumjibu kwa kuwa nilikuwa na pesa taslimu ya nauli yao mkononi mwangu kilichobakia ni kuwakabidhi tu. Baada ya mwendo kidogo gari hiyo ikasimama na kusheherekewa na vumbi kali nikashuka baada ya kulipa pesa yao, macho yangu yalipokewa na nyumba chache za nyasi huku nyingi zikiwa zimeezekwa kwa bati. Walijitahidi wakazi wa kijiji hiki japo nyumba zao hazikuwa zimejengwa karibukaribu, kuikaribia nyumba moja kutoka nyingine ilihitaji mwendo fulani. Kigiza kilikuwa kikianza kunukia nikatazama nilipotoka kisha nikatazama kule gari inakoelekea huku vumbi jepesi lililonilaki punde niliposhuka garini, likiwa linalifukuzia gari hilo kwa namna ya pekee. Niliitazama gari hiyo hadi ilipopotelea kwenye kona ndipo nikafanikiwa kuona kona moja mbele iliyokuwa inaelekea kushoto mwa barabara hiyo niliyopo, njia hiyo licha ya kutumiwa na waenda kwa miguu pia ilionekana kuwa ilikuwa ikitumiwa na magari japo ilizongwa na majani sana eneo la katikati. Nilipiga hatua mbele kuifuata ile njia huku nikiwaza kuhusiana na mtu niliyeambiwa ningemkuta mahala hapa. Nilipofika hapo kwenye njia hiyo mbele niliona gari ikiwa imeegeshwa kwa umbali wa kama Futi 50, nikalitazama kwa kina kabla ya kuanza kulifuata taratibu. Ilikuwa ni gari nyekundu ya kizamani sana kwa muundo wake ilijionesha, nilipokuwa nikizidi kulikaribia ndipo nilipogundua kuwa ni Peugeot 404. Ilikuwa imezimwa kabisa na hakukuonekana mtu eneo la karibu sikuacha kulisogelea kwani hata moyoni nilijikuta nikivutika kulifuata. Nilipobakisha hatua kama kumi hivi kulikaribia, nikatazama kupiti kioo cha kulia (Side mirror). Nikaona mtu kwa ndani na nilipokuwa nikimtazama vizuri, mlango huo ulifunguliwa kisha likatangulia buti kubwa la kijeshi lililofunika hadi ugoko kisha mzee mmiliki wa buti hilo akajitokeza na kusimama huku moshi mwingi wa sigara kutokea kinywani mwake ukitawanyika hewani, akageuka na kunitazama tabasamu likiwa usoni mwake kisha akanyoosha mkono kunipatia.




"Catherine wa Catherine!" Aliita huyo mzee ambaye bado mkono wake ulikuwa ukining'inia kuuhitaji mkono wangu. Nikampa mkono huku nikitikisa kichwa juu chini kukubaliana na jina aliloniita. Alipouachia mkono wangu nikakumbuka kuwa huyo alikuwa ni Luteni mstaafu wa jeshi hivyo nikajua niko na mtu wa namna gani.




"Karibu sana Ungamo, Karibu Asumile nyumbani kwangu taarifa zako ninazo." Aliongea huyo mzee huku akiwa ameung'ang'ania mkono wangu hapo ndipo nilikubali kuwa mzee huyu alikuwa mwanajeshi ambaye kustaafu kwake pia alilazimisha maana nchi bado ilikuwa ikimuhitaji japo umri wake ulimsimanga kuendelea kuwepo kazini. Mkono wangu ulikumbana na kashikashi kubwa sana kutoka kwenye mkono imara na uliokomaa na wenye nguvu pia wa mzee AKM. Niliutathmini umri wake alikuwa akikimbilia miaka sitini na tano ama sabiini hivi hata hivyo hakutimiza hata miaka mitatu tangu alipolazimisha ustaafu wake kwa kuandika barua yake moja kwa moja kwa muheshimiwa Rais kuwa sasa anaomba kustaafu maana umri unamsimanga sana ila akawa radhi kuwa pamoja kwa kila utakapohitajika uwepo wake. Na aliamua kupeleka malalamiko yake kwa muheshimiwa huyo kwa kuwa muheshimiwa huyo alipinga kwa kiasi kikubwa kamanda huyo kustaafu kwani mchango wake bado ulikuwa ukihitajika kwa kiasi kikubwa sana. Alikuwa imara mno.




"Asante nimekaribia Luteni mstaafu AKM." Nilimjibu nikimkabidhi ile bahasha ambayo hata hivyo hakuisoma aliitazama mgongoni mwake na kuikunja kisha akaitia mfukoni huku akiwa anauachia mkono wangu akaitoa sigara yake kinywani ambayo alikuwa ameibana na kingo zake za mdomo akapuliza moshi kwa madaha makubwa kisha akazunguka mlango wa pili na kuufungua nilielewa, hivyo nilielekea na kuingia upande ule akaufunga na kuzunguka upande wenye usukani akaingia.




"Mimi sikustaafu ni kama niko likizo tu maana kila wakati muheshimiwa Rais anataka kuniona utadhani mimi ndiye mkuu wa majeshi nchini." Alijibu huku akiivuta sigara yake na kukitupa kipisi nje akawasha gari na kuliondoa ukimya ukatawala garini mule macho ya AKM yakiwa makini na barabara hiyo mbaya. Tulitembea kwa umbali kidogo huku kimya kile kikiwa kikubwa, macho yangu yalikuwa yakitazama nje yakiitazama mandhari ya kijiji hicho ambacho kilitawaliwa na misitu ya hapa na pale, vichaka vilivyofungamana na nyasi nyingi wakati sehemu za tambarale zikitawaliwa na vichaka vidogo na mbuga ya nyasi fupi. Mandhari yake yalivutia kuyatazama. Wakati nikiwa nayatazama mandhari hayo, picha ya kutengeneza ya kifo cha Dokta Gabriel ikakivamia kichwa changu, sikuwa nimemuona wakati akiuawa hata hivyo nilijaribu kuhisi namna ambavyo aliuawa, nilimuona akiwa nyumbani kwake akiwa ametulia ndipo muuaji alimshtukizia na kumshambulia kwa risasi. Machozi yalinimwagika roho ikaniuma sana nikahisi mimi ndiye huwenda nilisababisha kifo chake, niliwaza na kuwazua, nikashika hili likaja lile. Nikafikiria mengi hasa kuhusiana na wanausalama ambao wapo kwenye mkasa huu wa kuwasaka au kusaka taarifa za madaktari waliyopotea. Huu ni mpango kabambe. Niliona bora niuite hivyo kwani kila hatua ilikuwa ikizaa kitu kipya. Hatua ya mwisho ni kifo kilichotokea mjini wakati nafika punde kutokea uwanja wa ndege.




"Kwanini uliamua kujiita Catherine wa Catherine?" Sauti ya AKM ilinitoa mawazoni na kunifanya nigande kwa sekunde kadhaa kabla ya kujibu.




"Mama yangu alikuwa akiitwa Catherine alikufa baada ya kunizaa mimi, mimi ndiye niliyemuua mama yangu labda niseme hivyo kwasababu alipatwa na kifafa cha mimba wakati akiwa anaelekea kujifungua mimi. Wasamalia wema waliomuokota akiwa barabarani akiomba msaada wa kufikishwa kwenye kituo cha afya walipata kusimuliwa machache na mama yangu kubwa alilokuwa akiwasisitizia ni mimi nitakapozaliwa nipewe jina la Catherine ili historia yake ya uchungu ibaki duniani kupitia mimi hata hivyo sikupewa historia ya baba yangu hii ilikuwa na maana kuwa wasamalia wale hawakupewa taarifa za baba yangu. Mama yangu hakutaka niijue historia ya baba yangu kabisa hivyo nikaamua kujiita Catherine wa Catherine kama mama alivyoagiza." Nilimjibu huku nikiyafinya macho yangu na mkono wangu wa kulia ukikunja ngumi kuashiria kuwa nilikuwa kwenye maumivu makali sana kwani tangu kuingia duniani sikuwa nimefanikiwa kuiona sura ya mama sawia zaidi ya kwenye picha. Hili bilashaka Luteni Abdallah Khalid Mapande aliliona hivyo akayatoa macho kwangu yaliyokuwa yakinitazama kwa kuibia kisha akayaelekeza mbele akiwa kimya baada ya kupumua kwa nguvu. Kimya kikatawala kwa muda huku gari likizidi kuchanja mbuga, tuliyapita mashamba kadhaa makubwa ya mazao mbalimbali, mbuga na vichaka vidogovidogo vilivyofungamana huku kigiza kikiwa kimeanza kupiga hodi.




"Kwanini unahisi muheshimiwa Rais wa nchi hii anapenda kukuona ukiwa kazini pamoja na umri wako kukukimbia kiasi hicho?" Niliamu kuuvunja ukimya kwa kumuuliza swali hilo. Hakuwahi kunijibu, alivuta fikira kwanza kisha akasema.




"Ukizungumzia watu waliyoitoa nchi pabaya lazima ndani yake unizungumzie mimi, tulipigana na kila lenye nia mbaya na nchi hii tukazitoa rehani roho zetu na kujitoa zaidi kuwasaidia wengine, tulipigana kwa jasho na kamasi hadi kuiacha nchi ikiwa dede kwa kiasi hiki. Wakati tukiwa mapambanoni kuna waheshimiwa walikuwa katika hali mbaya sana na walikuwa wakiandamwa kwa mabaya na ilhali ni watu wanaopenda na kutenda mema kwa taifa na wana taifa lao. Hawa ndiyo tuliyokuwa tukiwapigania kwa udi na uvumba hadi kuhakikisha wanakuwa sawa. Miongoni mwa watu hao alikuwapo muheshimiwa Rais wa sasa, sasa unadhani anaweza kuniacha niwe mbali wakati anaamini bado nina nguvu zangu?"




NJOO KESHO TENA TUJUE SABABU YA CATHERINE KUFIKA KWA AKM




HUKU NAKO TUNAMUONA CATHERINE AKIMUACHIA KADI YA MAWASILIANO JAMALI MAIGWA.








Wakati tukiwa mapambanoni kuna waheshimiwa walikuwa katika hali mbaya sana na walikuwa wakiandamwa kwa mabaya na ilhali ni watu wanaopenda na kutenda mema kwa taifa na wana taifa lao. Hawa ndiyo tuliyokuwa tukiwapigania kwa udi na uvumba hadi kuhakikisha wanakuwa sawa. Miongoni mwa watu hao alikuwapo muheshimiwa Rais wa sasa, sasa unadhani anaweza kuniacha niwe mbali wakati anaamini bado nina nguvu zangu?"




"Unaonekana kuwa bado uko vizuri ule ukakamavu haujakutupa mkono kama umri unavyokusaliti." Nilimwambia. Akacheka kwa nguvu sana hapa nikafanikiwa kuyaona meno yake yenye ukungu kiasi yaliyoathiriwa na moshi wa sigara kwa namna fulani japo weupe haukutoka kabisa, pia niliona pengo moja kwenye eneo la mbele la meno yake, jino moja lilimtoka pamoja na uzee alionao hata hivyo bado sura yake ilikuwa na haiba yenye mvuto wa kipekee sana. Nikavuta picha ya ujanani mwake huwenda alikuwa kijana mtanashati na jamali.




"Si sasa mwanangu, ukilinganisha zamani na sasa upo utofauti mkubwa sana japo kuwa nguvu zipo hata hivyo huwezi kunipambanisha na kijana imara wa leo." Alinijibu baada ya kumaliza kucheka. Nikamuona akipunguza mwendo wa gari baada ya kuingia kwenye shamba kubwa lililosheheni mazao mchanganyiko. Macho yangu yakaanza kuona kijani kibichi kilichoenda kwenye weusi baada ya giza kuingia kwa kasi. Japo giza la saa moja usiku lilikuwa likianza kuingia hata hivyo kijani kibichi hicho kutokea kwenye mimea mbalimbali iliyokuzwa kwenye shamba hilo haikujificha. Kulikuwa na Migomba mingi, michungwa, milimao, mindimu, miche ya mananasi ilikuwa imestawi sana, matikiti maji yalinawiri vibaya sana hadi nikashangaa kuona hali hii. Watu wanaishi shamba hata hivyo waliishi maisha bora kuliko wale waishio mjini. Niliona banda kubwa la kuku likiwa limesheheni kuku wa kutosha. Gari ilisimama sehemu iliyokuwa imeegeshwa gari moja la kizamani sana Toyota pickup kulikuwa na turubali kubwa jeusi likiwa limefunika kitu fulani mfano wa gari kama mbili ndogo. Alifungua mlango akatoka nami nikafanya hivyo sikutaka aje anifungulie tena kama awali.




"Karibu nyumbani binti?" Alinikaribisha, nilijizungusha kwa utaratibu sana nikitazama mandhari ya eneo hilo kwa utulivu mkubwa. Lilikuwa ni eneo la kuvutia sana, eneo hilo la maegesho ya magari lilikuwa limezungukwa na miembe ya kisasa na kienyeji, kulikuwa na mimea mingine ya matunda na miti mingine midogomidogo ya kivuli. Tulielekea pamoja kwenye jengo moja kubwa la kisasa lililojengwa imara kwa mawe kuanzia msingi wake, macho yangu bado yalizidi kutalii mandhari ile huku tukiwa tunaelekea ndani ya nyumba ile. Tuliingia ndani baada ya kufungua mlango akanikaribisha kwenye sebule pana iliyopangwa kistaarabu makochi matatu ya kisasa yalikuwa yameizunguka meza kubwa ya mbao, pembeni kwenye kona mbili kulikuwa na makochi makubwa ya kubeba watu wawili kila moja yakiwa yamepangwa usawa juu ya ile meza kulikuwa na kopo lililobeba Ua lenye mvuto kwa rangi zake mchanganyiko. Sebule ile ilikuwa imejengwa kisasa zaidi, dari yake ilisilibiwa kwa jipsam safi ya rangi ya maziwa ya kuvutia. Ukiwa ndani ya nyumba hiyo akili yako inakataa kuwa uko katikati ya shamba. Nilifikia kwenye kochi moja na kujikalisha nikatulia. Nilimuona akielekea kwenye friji moja lililopo hapo sebuleni pembeni kidogo ya kabati kubwa la vyombo. Akatoa chupa ya bia kisha akanitaka tutoke nje akidai sebuleni hapo palikuwa na joto sana. Sikumpinga nilijinyanyua kutoka kochini nikamfuata. Tulielekea kwenye kibanda kimoja kilichojengwa kwa nguzo moja chenye umbo la Uyoga na kilikuwa juu mfano wa Jukwaa, tulipanda kwa kutumia ngazi iliyounganishwa kwenye kibanda hicho hadi juu. Kulikuwa na viti vitatu vya kusukwa kwa magome ya mianzi vilikaa kiasili sana na vilivutia mno. Katikati kulikuwa na meza iliyotengenezwa kitaalamu kuizunguka ile kuzo na kuifanya meza hiyo kuwa na umbo la duara. Aliiweka ile chupa mezani na kuvuta kiti akaketi nami nilifanya hivyo.




"Mara nyingi niwapo hapa nyumbani napenda kukaa hapa kwani kuna upepo mwanana na naweza kuona eneo kubwa la shamba langu bila shida," alisema AKM huku akiitumia mikono yake kuonesha ukubwa wa shamba lake.




"Ni mazingira mazuri sana sijui hata ulifikiria nini kuja kukaa huku mwenyewe?" Nilimuuliza baada ya macho yangu kutalii eneo lile na kuona mazao mengine mengi ambayo sikuyaona hapo kabla. Alifikiri kwa muda kidogo Luteni mstaafu Abdallah Khalidi Mapande kisha akajibu.




"Uzuri ni kwamba sipendi kukaa sehemu yenye kelele, aghalabu huwa napenda kuwa mahala tulivu na pasipo purukushani nyingi. Naweza fanya mambo yangu kwa utulivu na nikafarijika."




"Ni sawa, nimeona Miwa kule bondeni na mimi ni mpenzi sana wa kumeng'enya miwa." Nilisema. Nilimuona Luteni Abdallah akimimina kinywaji kwenye bilauri yangu kisha akaifunga chupa ile na kunyanyuka akaniambia niendelee kupata kinywaji yeye akashuka zile ngazi na kuingia kwenye kibanda kidogo alipotoka alikuwa na kisu kikubwa kikali akielekea kwenye upande wenye bonde ambalo niliona miwa. Nikataka kumzuia kwa kuwa muda haukuruhusu hata hivyo nikaamua kujizuia na kubaki nikimtazama anavyotokomea shambani Muda mfupi baadae alirudi akiwa kifua wazi fulana yake nyepesi akiwa ameitundika begani huku mkono mmoja ukiwa umekamata kisu na Muwa. Alikuja akausimamisha pembeni kwenye kingo za kile kibanda kisha akajiweka kitini. Alikuwa na kifua kipana kilichojaa nywele nyingi zenye rangi nyeusi tii! Nilimtazama kwa kuibia huku nikiendelea kunywa.




"Wewe na mwalimu Dao mlijuana vipi Kamanda?" Nilitupa swali hilo baada ya kumuona amemaliza kuwasha sigara yake na kukitupia kiberiti mezani. Alinitazama kwa muda kidogo huku akiingia kwenye tafakuri nzito sana. Akapuliza moshi wa sigara yake hewani kisha;




"Si muda mrefu sana tangu kufahamiana kwangu na Mr. Daniel Matia Okale, kwa mahesabu ya haraka ni kama miaka mitatu au minne huko nyuma. Ilikuja taarifa kutoka moja kwa moja kwa Rais wa nchi hiyo na taarifa hiyo iliingia moja kwa moja Ikulu kwa muheshimiwa Rais Backa Ramson Backa. Taarifa hii ilikuwa ni ya siri sana na ilimtaka Rais wa nchi hii akubali kumficha Daniel Okale kwa muda wa miaka miwili hapa nchini huku huko Tanzania watu waliyokuwa na mpango mbaya wakiaminishwa kuwa amepoteza maisha. Ilistaajabisha na kwangu lilikuwa ni jambo geni hasa Rais alipoliita jopo la watu wachache waaminifu katiaka ngazi ya usalama wa nchi. Nilikuwapo mimi, alikuwapo mkuu wa kitengo cha upelelezi nchini, alikuwepo mkuu wa usalama wa taifa na pia alikuwepo makamo wa Rais. Likazungumzwa jambo hilo na kuibua mjadala mzito wengi wakalipinga na kusema si kama wanalikataa la hasha! Bali wanaohofu na jambo hilo kuwaingiza kwenye shida. Wazo likatoka kwangu ambalo liliwataka wajue walitakiwa kuisaidia nchi gani, niliwakumbusha jinsi nchi hiyo ilivyojitoa kulisaidia taifa hili ambalo kama si kutoa msaada wao pengine taifa hili lingeingia kwenye historia nyingine kubwa sana, wazo langu likawa na mashiko makubwa likaingia kwenye mjadala ambao ulichukuwa siku nzima hadi kufikia madhiimio. Rais alinitazama kwa jicho la pekee sana kwa sababu msaada huo kwa asilimia kubwa ulimuhusu yeye wakatia akiwa Waziri mkuu. Majadiliano ya jambo lile yakaafikiwa vizuri na majibu kurudishwa kwa Rais wa Tanzania kuwa limekubaliwa ombi kake. Wiki moja baade Mr. Daniel Matia Okale aliingia nchini hivyo Rais Backa akanikabidhi mtu yule na kuja kumficha huku shamba kwenye himaya hii. Tuliishi kama ndugu na tulikuwa tukizungumza mambo mengi kuhusiana na maisha haya tuishio. Nilikuwa nikija huku kila mwishoni mwa juma alinizoea sana na urafiki wetu ukakomaa na kuweka unasaba kabisa. Sishangai wewe kukuelekeza hapa na kukupa ujumbe ambao ulikuwa ni kama ushahidi tu ila mimi na yeye tulishalizungumza hilo." Alinieleza kwa mapana makubwa hii ikanifanya niione sababu ya mwalimu kunileta kwa huyu mtu, nilimtazama tena na tena kisha nikavuta bilauri ya kinywaji nikaweka kinywani nikapiga funda kubwa kisha nikairudisha mezani.




"Natumai safari yangu ya kuja hapa imepata mwangaza kupitia wewe, kuna mambo ya msingi ningependa unieleze na niweze kuondoka nayo maana sifikirii kuwa hapa kwa usiku huu....hii nchi ikoje Luteni?" Nilimuuliza baada ya kinywaji kile kushuka kooni vema.




"Nchi hii," akasema kisha akapiga kimya akafikiri kidogo kabla ya kujiweka sawa kitini na kuivuta sigara yake na kendelea huku moshi ukiwa umeipamba sura yake mithili ya jabali lililofichwa na ukungu.




"Haiko kwenye historia nzuri tangu hapo awali, imekuwa ikiandamwa na jinamizi baya la umwagwaji wa damu ambao ukiufuatilia kwa undani utagundua kuwa chanzo kikuu cha haya yote ni siasa. Siasa imekuwa ikilitafuna sana taifa hili, ugombanizi wa madaraka, tamaa ya viongozi wetu wa kiafrika kutaka kuongoza milele, imekuwa ni fimbo isiyo na macho ambayo viongozi wengi wamekuwa wakiikumbatia na kuifanya ndiyo muongozo wao."




"Hapo sijakuelewa Luteni?" Nilimwambia huku kichwa changu kikianza kuingia kwenye uchimbuzi wa kitu fulani, nilianza kuipata picha kamili ya kilichonifikisha Ungamo hata hivyo kilichokuwa kikinitatiza ni namna ambavyo haya mambo yalivyokuwa yameingiliana.




"Nisikilize vizuri nadhani unaweza kuipata picha halisi ya hiki nikisemacho hasa kuhusiana na swali lako. Mataifa mengi ya bara letu la Afrika viongozi wake ni wingi wa tamaa ya madaraka, wapenda mali, na tamaa ya kuitwa watukufu milele. Hili ndilo wanaloliabudu zaidi kuliko kitu kingine chochote na kuwafanya wapende kukaa madarakani muda mrefu kama wafalme, wapo viongozi ambao maisha yao yote wanataka kuishi kwenye uongozi hadi siku wanaingia kaburini. Wanaamini kufa ukiwa kiongozi ni heshima kubwa mno kiasi cha kuweza kukaa kwenye majalada makubwa ya vitabu vya wanaharakati na wachambuzi wa masuala ya siasa huku historia zao zikiwa ndizo zinazoshika kurasa za makala mbalimbali. Utajiri wa kujilimbikizia mali ilhali wananchi wake wakitaabika na umasikini usiofika kikomo. Hili ndilo jinamizi linaloitesa Afrika. Jinamizi hili lipo kila mahali, hapa Ungamo hili lipo na ndilo linaloiingiza nchi hii kwenye matatizo na migogoro mikubwa isiyokwisha na mifano hii ipo...ipo Catherine, tumeona kwa Rais Mugabe, Piere Nkurunzinza waliong'ang'ana hata kutaka kubadili katiba ya nchi ili iendane na matakwa yao na mengine mengi. Fimbo waliyoikumbatia au wanayoikumbatia, ndiyo inaamsha umwagikaji wa damu, kutokuaminiana hata kuzushiana mambo yasiyo na maana au yenye kuleta uchochezi mbaya unaosababisha hatari yenye kuangamiza.....!" Aliweka tuo Luteni mstaafu baada ya kuongea hayo akapiga funda moja la kinywaji kisha akaibana sigara yake kwenye kingo za midomo yake na kuivuta. Aliutoa moshi nje kwa madaha akanitazama na kuendelea.




"....fimbo hiyo ndiyo wanayoitumia mabepari wa huko ughaibuni kuiharibu demokrasia ya Afrika au niseme ndiyo iliyoiharibu amani ya nchi hii kwa asilimia kubwa sana na haijulikani itarudi kwa namna gani. Wanatumia pesa kama fimbo isiyo na macho. Pesa hizo zinapomwagwa kwa kila kiongozi hakuna masilikizano maana kuna baadhi ya watu wanakuja kujiona wako juu kuliko mtu yeyote yule. Mabepari hawa si wajinga, wanafanya hivi ili iwe rahisi kwao kuchota kila kilichomo ndani na kutoka nacho nje na kwenda kujifaidisha kwenye mataifa yao na mwafrika anabaki kuwa mpiga kelele asiye na kituo maalumu. Hawa viongozi wetu wa ki-Afrika wanaopewa pesa hujiona hakuna mwenye nguvu dhidi yao, hakuna mwenye kutia neno hata moja na akijitokeza wa kufanya hivyo hapa ndipo inapoibuka vita na vita hii inakuwa mbaya sana kwasababu unayekwenda kupambana naye anakuwa na nguvu kuliko mwingine yeyote. Umeona jinsi migogoro inavyoibuka kwenye nchi hizi za ki-Afrika pasipo kujua hiyo fimbo ni mbaya na baada ya hapo ni kuwarudia wenyewe na kuja kudai fidia kwa kigezo cha kuwasaidia hadi kushika nyadhifa mbalimbali. Ikifikia hapa nchi inakuwa utumwani pasipo kujua nani ni waingizaji wa taifa hilo utumwani, raia wa hali ya chini ndiwo pekee watakao kula joto la jiwe huku wachache wakikuna vitambi kwenye mahoteli ya nyota kuanzia nne kwenda juu.....!" Akaweka kituo tena na kuvuta sigara yake kisha akatulia kwa jozi ya sekunde na kunitazama usoni kama anayesoma kitu kutoka kwangu au akitathmini usikivu wangu au upokezi wa kile akizungumzacho. Akaendelea.




"....taifa hili lilipandikizwa watu wa namna hiyo tangu mwanzo lengo kuu likiwa ni kuharibu kabisa amani ili wachache wafaidi, kwenye hili viongozi wetu wenye tamaa walikuwa wazi kuua wengine wanaoweka kauzibe na hawakujali maumivu ama machungu yatakayopatikana kwa watu wa chini. Nguvu kubwa ikatumika na viongozi wachache waaminifu wakasimama imara hawakujali familia zao wala nini, hawakuogopa maumivu yatokanayo na mateso makali waliyoyapa pia walipuuza kwa machungu damu zao na za familia zao zilivyokuwa zikimwagika...lengo ni nini..? Lengo ni ukombozi, lengo ni kulirudishia taifa amani ya kweli...! Walihakikisha kila mwenye nia chafu anasambaratika na kuliacha taifa hili kwenye mikono salama, kwa hili nampongeza sana Rais Mabandu ambaye alipambana kwa kila hali, hakumjali mkewe wala bintiye na maumivu makali aliyavumilia hadi kumuadabisha Kiongozi Haini Julio Mobande Julio wa kipindi hicho cha nyuma kabla yake, jina lake litazidi kukumbukwa sana....!"




"Unataka kuniambia hii nchi imetuama na hakuna shida tena?" Niliuliza swali ambalo majibu yake sidhani kama yako sahihi kichwani mwangu hata hivyo nilikuwa na maana kubwa kuuliza kwa namna hiyo.




"Nchi bado haiko shwari na kwa hili nikuambie binti, wanausalama wako kazini kuhakikisha nchi hii inakaa kwenye amani iliyo kamili kwani mauaji ya viongozi waliopita yanatokea kila leo nimepata taarifa kuwa tayari wamemuua mkuu wa kituoa kikuu cha polisi."


ITAENDELEA


imulizi : Mpango Wa Nje - Ni Pigo Butu La Kifo 


Sehemu Ya Tatu (3)






"Kweli Luteni usemalo napata mashaka sana kuhusu kazi yangu iliyonileta huku, hofu hii ni kuhusu kuingiliana na jambo jingine ambalo si ndani ya kilichonileta?" Nilizungumza nikiwa makini zaidi. Akanitazama Luteni Abdallah Khalid kisha akaibana sigara yake kwenye kingo za midomo na kuivuta huku mimi nikiutumia mwanya huo kuongeza kinywaji kwa kiasi kidogo sana kwenye bilauri. Akapuliza moshi nje akasema.




"Fanya kilichokuleta." Likikuwa ni jibu fupi na lililoficha muendelezo mzito.




Nifanye kilichonileta. Niliwaza. Hii ilikuwa na maana kuwa niendelee na kazi niliyotumwa na nchi yangu ya kuwatafuta madaktaktari waliopotea nchini Tanzania na kusemekana wameingizwa nchini hapa ila wasijulikane wako wapi.




CATHERINE FUATA KILICHOKUPELEKA UNGAMO.






Akanitazama Luteni Abdallah Khalid kisha akaibana sigara yake kwenye kingo za midomo na kuivuta huku mimi nikiutumia mwanya huo kuongeza kinywaji kwa kiasi kidogo sana kwenye bilauri. Akapuliza moshi nje akasema.




"Fanya kilichokuleta." Likikuwa ni jibu fupi na lililoficha muendelezo mzito.




Nifanye kilichonileta. Niliwaza. Hii ilikuwa na maana kuwa niendelee na kazi niliyotumwa na nchi yangu ya kuwatafuta madaktaktari waliopotea nchini Tanzania na kusemekana wameingizwa nchini hapa ila wasijulikane wako wapi.




Hii ilikuwa na maana gani? Na ikiwa nimekaribishwa na kifo cha mtu ambaye alikuwa ni mwenye cheo kwenye jeshi la polisi. Mkuu wa kituo kikuu cha polisi Muavengero...? Je, kama wanaoendeleza matukio haya ni haohao waliyohusika na utekaji wa madaktari wetu...? Niliwaza. Sikutaka wazo hili nikae nalo na niondoke nalo. Nililitengenezea swali na kumpachika Luteni mstaafu kuhusiana na hilo lihusianalo na kifo cha Mansuli Bingwa kama alivyoniambia AKM.




"Habari za kifo cha mkuu wa kituo cha polisi Muavengero Kamanda Mansuli Bingwa ni kazi mbichi iliyoibuliwa kutoka kwenye ile iliyopoa. Zingelikuwa ni enzi zangu damu ingenichemka sana." Alinijibu jibu jingine tata, nikabaki kwenye utata. Nikamtazama kwa tuo nikapata picha kamili kuhusiana na huyu mzee na kwa kiasi fulani nikaanza kujua ni kwanini Rais Backa Ramson Backa alizidi kumng'ang'ania. Haridhiki na anachokiona kwa macho, hupenda kuchimbua mambo na pia anajiamini kuliko wengi wanavyojiamini. Kama ningemuuliza swali kuhusiana na jambo lile huwenda tungekesha na bado nisingeuliza swali hata moja juu ya kile kilichoniingiza kwenye nchi ya Ungamo.




"Ulishawahi kulisikia jina la mtu anayeitwa Musa?" Nilimuuliza huku nikiitazama saa yangu ya mkononi ambayo ilinitanabaishia kuwa ilipata saa mbili usiku. Taa kali za kung'aa zilizokuwa zikiwaka hapo kutuangazia zilikuwa zikituhadaa na kuamini muda ulikuwa pamoja nasi kumbe ilikuwa kinyume chake. AKM alielewa maana yangu ya kutazama saa naye akatazama ya kwake huku akiisiga ile sigara kwenye meza kisha akakitupia kipisi nje ya kile kibanda. Ulikuwa ni utaratibu wa kiporipori, hakujali.




"Musa!" Akaanza kwa kulitaja kisha kuyanyanyua macho yake na kuyaning'iniza kwenye paa la nyasi la kile kibanda chenye umbo la uyoga. Tafakuri ilikuwa kichwani mwake. Alishusha pumzi nyingi tokea kifuani mwake na kushindana kutoka kwenye tundu mbili pana za pua yake zilizosheheni vinyweleo vya kutosha.




"Nimekuwa nikilisikia sana jina hili ila sidhani kama huyu mtu yupo hai," nikashtuka.




Kwanini adhani hivyo? Nikajiuliza kisha nikaukusanya ubongo wangu na kuutoa nje kisha nikazichukua fikra na kuzitawanya kwenye fuvu la kichwa ili zitafakariwe kwa undani. Ilikuwa ni miaka mingi imekatika tangu jina Musa lipate kuwa maarufu na kubandikwa kama ushahidi kwa hati ya mkono kwenye moja ya karatasi za kiuchunguzi za Dokta makini Dokta Lumoso Papi Mmbai.




Miaka ishirini imekatika sasa. Huwenda Musa akawa amefariki kweli...? Nikajishauri. Nikawaza kuhusiana na madaktari ambao kwa kipindi hiki wangekuwa na umri sawa na wa marehemu Dokta Gabriel Nyagile aliyeuawa kwa hila. Nilipatwa na uchungu sana nilipomkumbuka Daktari Nyagile. Roho iliniuma sana na kujiuliza kwanini hata sikujisukuma kwenda nyumbani kwake walau kuyaona mazingira ya kifo chake hata hivyo nikajipa utulivu wa nafsi, sikuwa na namna nyingine sasa zaidi ya kuapa kuunganisha matukio hadi nimjue aliyehusika na kifo hicho.




"Huwenda hata ninaowatafuta watakuwa si watu hai?" Nilimuuliza AKM huku nikiendelea kumtazama usoni kwa umakini. Hakunijibu kwa haraka pia hakukawia.




"Narudia tena binti, fanya kilichokuleta." AKM alinijibu huku akiitazama saa yake akasimama na kuiokota fulana yake akaitupia begani tena. Alikuwa akitumia amri za kijeshi za kuvunja mazungumzo baada ya kuona ningali na maswali mengi. Akapiga hatua mbili akiwa anazielekea ngazi za kushukia chini, nikavunja shingo kumtazama.




"Kazi yako utaifanya ukiwa ndani ya mji tulivu wa Ashura, mji huu si kama hauna majengo mengi bali ulikuwa ni mji wa kistaarabu tangu hapo na ukaishi na kudumu kwenye ustaarabu huo, ukimya ndiyo sababu kuu ya kutaka uishi hapo hadi pale kazi yako itakapokwisha, usiri wa kazi yako ndiyo sababu kuu sipendi uiharibu. Utaanzia kazi yako ukiwa kwenye jengo la maficho la hapo mjini kutokea Hoteli kubwa ya nyota nne ya Amala Bay. Ni mita mbili kutoka ilipo Hoteli hadi jengo hilo. Kila utakachokikuta ndani ya jengo hilo ni chako na kitakuhusu au kuhusiana na kazi yako." Alimaliza kuongea AKM kisha akashuka zile ngazi kwa mwendo wa kukimbiakimbia. Nikanyanyuka kisha nikaokota ule Mua nikahesabu pingili sita kisha nikauvunja kwa kuugandamiza kwenye goti langu. Uliobakia nikauacha pale chini kipande cha pingili sita nikiteremka nacho nikimfuta mzee yule mkakamavu. Tulisimama kwenye lile turubai jeusi mahali alipopatenga kama maegesho ya magari. Hakusema na mimi alivuta kamba mahali na kufungua kisha akalivuta lile turubai. Kulikuwa na gari mbili zote za aina moja zilitofautiana rangi tu. Zilikuwa ni gari za kizamani Peugeot 404 moja ya rangi nyeupe na nyingine ikiwa ni ya rangi nyekundu iliyoiva. Zilikuwa zikiwaka kwa rangi yake. Jumla huyu mzee alikuwa na gari za aina hiyo tatu hizo mbili na ile aliyoitumia kunipokelea mimi huku moja ikiwa ni Toyota Pickup. Akanitazama.




"Utachagua itakayokufaa," aliniambia. Sikumjibu bali niliisogelea Peugeot ya rangi nyekundu kisha nikaitazama. AKM alinitazama akaachia tabasamu huku akienda kwenye ukuta akavuta kitasa kutoka kwenye kiboksi cha mbao ya mvuje kilichopo juu ukutani akavuta kikasha kimoja cha funguo za gari akakifunga kile kiboksi na kunigeukia akizirusha zile funguo nami nikazidaka.




"Nilijua ungechagua gari hiyo maana hakuna rangi inayovutia kwa mabinti kama nyekundu sijui hata mnavutika na nini?" Alisema akiwa ananisogelea. Nikautazama mwendo wake na kuyatazama magoti yake namna yanavyojikunja na kujikunjua, unaweza kusema aliwahi kutembelea magongo baada ya kuvunjwa vibaya miguu yake. Alikuwa na mikogo katika kutembea kama Van Dame.




"Navutiwa na rangi hii tangu nikiwa mdogo na nakumbuka nilipewa jina la bikini nyekundu kwa kuhusudu kuvaa vitu vya rangi hiyo." Nilimjibu nikiwa natabasamu. Akatabasamu pia kisha akasema.




"Mwanzo mwema wa kazi yako. Tutawasiliana ukifika kwenye jengo hilo." Aliniambia akinikabidhi ramani ndogo ambayo ilinionesha kuanzia Hoteli ya Amala Bay japo haikuwa na umuhimu sana kwangu kwa kuwa nilikuwa nayo ramani yangu ya kijasusi ya nchi nzima ya Ungamo hata hivyo sikuiacha. Jumba hilo lilikuwa upande wa kaskazini mwa mji huo wa Ashura ndivyo nilivyoiona kupitia ile ramani aliyonipa AKM. Niliingia kwenye gari baada ya kuhakikisha mafuta yaliyomo yalikuwa ya kutosha kisha nikaliwasha nalo likaunguruma kama simba, likanipa raha nikaliondoa kwa kasi mwanga mkali wa gari hiyo ulinipa jeuri ya kuitazama njia vema kuliendesha gari hilo vile nitakavyo.




_________




Saa mbili usiku vijana wawili walikuwa wakiingia ungamo kutokea nchini Tanzania na hawa walikuwa wameingia nchini hapa nyuma ya mwanadada Catherine. Mwambije mkami alidhamiria kuhakikisha kazi yake aliyopewa na mkuu wa nchi haifeli hivyo mara baada ya vijana kurudi tokea Morogoro, alichambua chunguzi zao na kwenye chunguzi hizo akapata kujua ni wapi alitakiwa kuendelea napo. Akaunganisha na chunguzi zilizowahi kufanyika huko nyuma haraka sana akapata kujua alipotakiwa kuwaagiza vijana hivyo akatoa amri kuwa safari iwe ni ya nchini Ungamo na si vinginevyo. Vijana hao miongoni mwao alikuwa ni Sembuyagi Mpauko Haufi akiambatana na Mabule huku kwenye kikosi chao akipunguzwa Jackson. Walipotoka uwanja wa ndege wa Tao De, moja kwa moja walichukua Hoteli mjini na kuupitisha usiku huo ili kuchapo waweze kukutana na mtu waliyetakiwa kukutana naye na wajue namna ya kuanza kazi yao vema. Vijana hawa walikuwa na ari kubwa sana ya kufanya kazi na kuhakikisha madaktari waliopotea miaka mingi huko nyuma wanapatikana hata mifupa yao. Usiku huu hawakutaka kuisumbua miili yao vilevile hawakutaka kukurupuka pasipo kuwa na maamrisho toka kwa mtu ambaye wangekutana naye siku itakayofuata.




Wakati vijana hawa wakiwa wanautafuta usingizi, muda huohuo Frank Matiale Bambi alikuwa macho makavu kabisa akifunua hapa na pale huku na kule, akizidi kupekenyua aweze kupata walau pa kuanzia safari yake. Bado alikuwa akifikiria namna ambavyo angefanya ili kuujua undani wa kifo cha kamanda Mansuli Bingwa. Alitafakari mengi kuhusu kifo kile hata hivyo akakata shauri mwishoni mwa mafikirio yake na kuona ni vema kuchapo arudi tena kwenye soko lile na aanzie hapo upelelezi wake. Huwenda kupita hapo kuna mwanga ambao angeweza kuupata na kujua jinsi itakavyokuwa rahisi kujua nia thabiti ya mauaji na wauaji wale. Ilikuwa ni ngumu sana kuamini kama angeweza kufanikiwa hata hivyo hakuona sababu ya kuyapinga mawazo yake. Akafunga upekuaji wake akakisogelea kitanda akakaa juu yake kisha akajipandisha akazima taa kupitia swichi iliyokuwa ikining'inia juu kidogo ya kichwa chake akaliruhusu giza akayafumba macho yake akiutafuta usingizi wa mang'amng'am.




_________




Ilikuwa inapata saa mbili na dakika thelathini na ushei, utulivu haukufua dafu kupenyeza makucha yake kwenye fujo za asubuhi hiyo ndani ya soko kuu la mjini hapo. Kelele za wachuuzi wa mboga, matunda, vyakula, madawa ya asili, vyombo viumbwavyo kwa udongo (vyungu na kadhalika). Mafagio na kadha wa kadha zilichangamana na kelele za wanunuzi wa bidhaa hizo sambamba na washusha mizigo ya wachuuzi kutoka kwenye malori kadhaa yaliyosimamisha gurudumu zake kwenye lango kuu la kuingilia sokoni hapo. Muda huu ulikuwa ni wa purukushani sana hivyo kelele ikawa na nafasi kubwa kuliko chochote. Frank Matiale Bambi alinyanyua mkono wake wenye saa na kutazama muda, bado ilikuwa ni mapema. Akaushusha mkono wake uliobeba saa na kuutia mfukoni mwa suruali akatoa miwani ya kioo cheusi yenye uwezo mkubwa sana wa kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja hasa pale tu utakapoamua kuiagiza ifanye hivyo. Ilikuwa na uwezo wa kuona kwa umbali wa mita zaidi ya mia mbili na kwa ufasaha gizani, ilikuwa na uwezo wa kupiga picha mnato na kupenyeza uoni wake hata mbele ya kioo kigumu kisichoruhusu kuona ndani, akaipuliza vumbi miwani hiyo kiasi na kuipachika machoni kisha mkono huu usio na saa akautia kwenye mfuko mwingine wa suruali alipoutoa mkononi alikuwa na vijiti viwili vya kuchokonolea meno (Toothpick). Akakirudisha kimoja mfukoni na kile kimoja akakipachika kinywani sina hakika kama ulikuwa ni utaratibu aliouibua au kuna kitu kilichokuwa kikimpa ghasia kwenye meno yake kwani hakuwa na upendeleo au mazoea ya kufanya hivyo.




Bado mapema utulivu haujawa mzuri bado. Akajishauri moyoni kisha akapiga hatua za taratibu hadi ulipo mgahawa mmoja wa wazi ambao ungemuwezesha kuona nje. Akiwa hapa alikaribishwa na muhudumu wa mgahawa huo. Alikuwa na njaa na alitaka kutia japo kitu mwilini wasaa huu ulikuwa mzuri na ungemuwezesha pia kuvuta subira ya muda autakao.




Aliagiza alichotaka kuletewa akasubiri na punde kukashuka supu ya Jodari na chapati mbili nzito kukiambatana na kikombe kirefu kinene cha maziwa ya moto yaliyokuwa yakifuka moshi. Alinawishwa mikono kisha kabla ya kula akapiga alama ya msalaba akikipachua kile kijiti kinywani na kutupia macho nje akitazama kwenye lango la kuingilia ndani ya soko. Bado watu walikuwa wakiingia na kutoka, akayarudisha macho yake kwenye mlo akahamisha fikra zake hapo na kuushambulia mlo huo wa kufungua kinywa na baada ya muda mfupi baadae akawa anatazamana na vyombo vitupu. Akanawa maji kisha akapachika kijiti kingine kinywani baada ya kumaliza kula huku akichokoa meno yake taratibu kabla ya kukitupa. Akatazama saa yake ikamwambia kuwa ilikuwa ni saa tatu sasa na uchafu mdogo wa dakika. Akalipa alichopaswa kulipa akatoka hapo taratibu.




Alikuwa amevaa suruali ya jeans ya rangi ya buluu iliyoiva, juu alitupia shati la mirabamiraba ya rangi nyeusi na nyeupe huku kwenye mkatisho wa miraba hiyo kukipita mistari ya rangi ya manjano mpauko pande zote. Miwani yake ya jua ilikuwa machoni mwake, rasta nyeusi tii! Zilizosokotwa na kusukwa vema kichwani zilimuweka kwenye muonekano wa tofauti sana na wa kupendeza. Chini alivaa raba nyeupe zenye chapa ya Nike. Alifika kama mnunuzi kwenye soko lile kisha akaanza kuangaza macho yake huku na huko akitafuta mahali pa kuanzia. Akili yake ilijaa picha ya tukio zima lilivyokuwa hata kama hakuwa shuhuda lakini kupitia kwa mahojiano machache aliyoyafanya ni wazi alikuwa na kitu kichwani mwake. Akatazama kizimba kimoja kilichokuwa kimejaa bidhaa mchanganyiko. Akavutiwa na kizimba hiki, si kama alivutiwa kwa sababu ya mchanganyiko wa bidhaa zilizopo hapo kizimbani la hasha! Kizimba hiki kilikuwa karibu na ukuta mfupi wenye kumuwezesha muuzaji wa kizimba hicho kuona nje kwa ufasaha. Alipiga mahesabu ya kutosha sana kabla ya kuamua kukisogelea kizimba hicho. Hatua kama kumi za mtu mzima mwenye urefu wa futi tano na nusu zilitosha kumfikisha mtu huyo kutoka hapo kizimbani hadi lilipotokea tukio la mauaji. Kama mchuuzi wa kizimba hicho alikuwapo wakato tukio la mauaji likitokea, ni wazi alishuhudia kila kitu kilichokuwa kikiendelea ama kilichotokea.




Patanifaa hapa kuanzia! Akajishauri. Akamtazama mmiliki wa kizimba hicho ambaye alikuwa ni mzee mfupi kiasi mwenye kitambi cha wastani kilichofunikwa na vazi la Kanzu safi ya rangi ya chokoleti huku vazi hilo likitendewa haki na kofia ya 'balakhashee' iliyopo kichwani mwake.








Kama mchuuzi wa kizimba hicho alikuwapo wakato tukio la mauaji likitokea, ni wazi alishuhudia kila kitu kilichokuwa kikiendelea ama kilichotokea.




Patanifaa hapa kuanzia! Akajishauri. Akamtazama mmiliki wa kizimba hicho ambaye alikuwa ni mzee mfupi kiasi mwenye kitambi cha wastani kilichofunikwa na vazi la Kanzu safi ya rangi ya chokoleti huku vazi hilo likitendewa haki na kofia ya 'balakhashee' iliyopo kichwani mwake. Alikuwa mcheshi kwa muonekano na kupitia matamshi yake aliyokuwa akiongea na kijana mmoja wa kizimba kingine huku akihangaika kupima kilo ya Karanga mbichi, ilimpa sifa ya mpenda utani na muongezi sana. Alikuwa na ndevu kidevuni zisizo ndefu wala fupi zenye rangi mchanganyiko wa weusi na weupe ulioanza kutawala hata hivyo kwenye mfuko wa Kanzu yake kulikuwa na kimkebe cha kuhifadhia miwani ya kusomea. Matamshi yake yaliyojiingiza kwenye maongezi yake yalimvunja mbavu yule kijana na wateja wawili aliokuwa akiwahudumia na yeye alikuwa mkavu kama hakuwa yeye msulubu wa mbavu za wenzake kwa vicheko. Frank Bambi hakuwa na papara alikuwa akipita hapa na pale akitazama hiki na kile ili kupisha mzee yule amalize kuwahudumia wale wateja ndipo asogee. Aliposalia mteja mmoja ndipo Frank alipojisogeza kisha akamkaribia kabisa akipishana na yule mteja aliyekwisha kuhudumiwa.




"Shikamoo mzee?" Alidumisha mila za kiafrika Franki Matiale Bambi.


"Marahaba, karibu kijana?" Aliitika uamkuzi huo mzee huyo kisha akaendelea kuviremba vichuguu vya bidhaa zake zilizosheheni kwenye makapu kama Karanga mbichi, Kunde, Choroko, Mbaazi, Maharagwe, Mchele, Ulezi, Mtama, Uwele, Unga wa dona, Mahindi yaliyokobolewa, Njugu mawe, Chumvi ya mawe na kadhalika. Frank alikitazama kizimba kile jinsi kilivyosheheni bidhaa nyingi za kumvuta mteja kulingana na hitaji lake.




"Asante sana mzee wangu?" Aliitikia ukaribisho kisha akavuta pakiti moja ya unga wa mdalasini akauminyaminya na kuuliza bei.




"Pakiti hiyo ni shilingi elfu moja tu kijana." Akajibu yule mzee.




"Asali nayo ni bei gani?" Akauliza Frank Matiale huku akiwa anaiachia mezani ile pakiti ya unga wa Mdalasini.




"Asali ipo kwa bei tofauti, ipo hii ya kwenye chupa ndogo ambayo nauza kwa bei ya shilingi elfu mbili na mia tano, hiyo inayofuata ni shilingi elfu tatu na mia tano hata hivyo ipo hiyo ya kwenye chupa ya lita moja na nusu ya nyuki wadogo ambayo bei yake ni shilingi elfu kumi na mbili." Alieleza bei huyo mzee kisha akamtazama Frank usoni.




"Nimeona hapo kuna juisi ya vitunguu saumu nayo unauzaje?" Akauliza Frank huku akimtazama mzee huyo kwa macho ya udadisi, kulikuwa na kitu alikuwa akikichimba kwa mzee huyo huku lengo kuu likiwa ni kumleta kwenye maongezi. Mzee huyo alitabasamu kisha akajibu kuwa juisi ya vitunguu saumu bei yake ni shilingi elfu mbili.




"Nakuona unatabasamu mzee wangu huku ukinipa bei?" Akachokoza Frank.




"Kijana naona lengo lako ni nini hapa, ni vema ukija sehemu kama hizi uulize. Hapa hakuna kinachokosekana bwana tuko wazee wachache sana hapa ambao tunauza vitu adimu kama hivi. Mdalasini mwenzake Asali tena upate asali mbichi ya nyuki wadogo, juisi ya vitunguu saumu ukiichanganya na maziwa freshi yatokayo kwa ng'ombe moja kwa moja bila kupitia kiwandani, shughuli yake wanaijua wakina mama na wazee wanaotumia bidhaa hii hata vijana hawapigi nyanga kwa wake zao. Heshima ipo....!" Akaweka kibwagizo kisha akatulia kidogo akimtazama mteja wake kwa tabasamu la kumkarimu zaidi kisha akauvunja tena ukimya.




"....nadhani unataka tiba ya kufuli la kumfungia mama asitoke ndani kwa kisingizio cha muwasho. Umepata. Wananiita mzee wa inatosha, kwa jina maarufu Aliwatani Mahamdu!" Akajipiga ufagio mzee kwa tambo za kuzidi kisha akamueleza Frank kinagaubaga namna ya matumizi ya bidhaa hizo sambamba na shughuli yake baada ya kutumia. Frank akamtazama Aliwatani Mahamdu kwa udadisi mkubwa huku tabasamu la matumaini likiwa usoni mwake. Alifanikiwa kumvuta mzee kwenye lengo. Hakuona uvivu kuwapisha wateja wajao wahudumiwe yeye akisimama kwa minajili ya kuhitimishiwa utumizi wa bidhaa aitakayo.




Alitazama nje kwa mara nyingine kupitia ule uwazi, akatazama mahali gari ya marehemu kamanda Mansuli Bingwa ilipokuwa siku iliyopita alipolishuhudia tukio la kuuawa kwake kisha akatazama mahali gari ya wanaohisiwa kuwa ni washambulizi au wauaji wa marahemu Mansuli ilipokuwa pia. Hapakuwa mbali sana na maono ya mtu ambaye alikaa hapa karibu na huu ukuta wenye kuruhusu kuona nje. Wateja walipoondoka akamtazama tena Mahamdu.




"Utanifungia hivi hapa ambavyo tumeweka hapa kando....bila shaka unawateja wengi sana vijana na wazee wenye shida na heshima kwenye ndoa zao?" Aliuliza Frank Matiale Bambi akiwa anachomoa waleti yake kutoka mfukoni.




"Sana kijana, sanaa...! Unajua si kwamba vijana ni wabovu wawapo kwenye uwanja wa starehe ya ndoa lah! Wanachoamini vijana wa sasa ni kwamba wanawake hawaridhishwi na kile wapewacho na wapenzi wao sasa kuwapo na vichochezi na viimarishi vya kudumu kwa muda mzuri kifuani kunawafanya wahisi raha mara dufu na kuwafikisha kileleni pasipo kurudia mzunguuko. Hata unapokuja kurudia mzunguuko tayari mwanamke ameshakuheshimu na kukuacha uende bila kukuudhi akikusindikiza kwa furaha katika kumpeleka kilele kingine cha mafanikio ya safari yenu. Unajua hata watu na nyadhifa zao wanakuja hapa na wanachokipendea kwangu ni darasa kabla ya huduma." Aliongea mzee Mahamdu kisha akaufunga mfuko baada ya kuvitumbukiza vitu vyote vilivyotakiwa.




"Unataka kuniambia hata watu wakubwa na nyadhifa zao wanakuja sana hapa?"




"Haswaa! Kijana usitake kunichekesha (akacheka pamoja na kuomba asichekeshwe). Hata marehemu Mansuli Bingwa aliyeuawa hapo nje ya soko hili alikuwa mteja wangu mkubwa sana. Siku ile alitoka hapa baada ya kumaliza kuchukua bidhaa nyingine...!"




"Aisee halafu kweli kabisa mzee wangu, niliipata hiyo taarifa punde tu nilipofika hapa mjini jana kutokea Sami Ado. Nasikia alipigwa risasi na watu wasiofahamika?" Frank Matiale Bambi alimkata mzee huyo kauli na kuifanya sentesi yake kuogelea hewa akamuuliza kwa mitego.




"Hukupata kushuhudia?" Akauliza hata hivyo hakusubiri jibu.




"Si jambo la kuzungumza polepole hilo," akaendelea mzee Mahamdu.




"Mansuli Bingwa kabla ya kutoka hapa nilipomaliza kumhudumia alikuwa akitazama sana nyuma yangu, hakuwa mcheshi na mchangamfu kama nilivyoielewa tabia yake, aliukumbatia upole na ukimya kwa hali ya juu sana. Nilipogeuka nyuma kutazama atazamacho nikaona gari ndogo ya rangi nyeupe ikiwa imeegeshwa umbali wa kama mita hamsini hivi kutokea hapa. Alikuwa akiitazama sana gari hiyo ambayo ilikuwa ni Toyota Vitara yenye namba za usajili U 768 AB. Ni kama aliyekuwa akiitilia mashaka ile gari hata hivyo hakuna aliyehangaika kumuuliza alinikabidhi pesa nami nikampa bidhaa yake kwa kuwa nilikuwa nikimfahamu na kulifahamu hitaji lake awapo hapa labda kuwe na ziada. Akaondoka na kulifuata gari lake akaingia na kujituliza kimya kwa dakika nyingi bila kuondoka. Wapo waliyoniuliza hapa kuhusu masaibu yaliyompata mteja wangu hata hivyo sikuwa na jibu jingine zaidi ya lile la hata mimi nashangaa. Macho yangu yalikuwa yakilitazama lile gari ambalo kwa usawa lilikuwa likitazamana na gari la Mansuli. Kwa macho yangu kijana nilishuhudia mtutu wa bunduki ndefu ukichungulia kwenye dirisha la ile Toyota Vitara kisha mlipuko mkubwa na sauti ya mpasuko wa kioo cha gari ya Mansuli Bingwa vikasikika vikipishana kwa nukta chache tu. Gari ile ilipoteza sekunde zipatazo kumi tu na kuserereshwa kabla ya kutokomea barabarani." Alihitimisha mzee Mahamdu huku akimtazama Frank usoni ambaye alikumbwa na fadhaa kubwa sana baada ya kusikia simulizi hiyo. Moyo wake ulitabasamu baada ya kupata picha kamili ya kuanza nayo. Ilikuwa na maana gani simulizi hiyo kwa jinsi ilivyoanza hadi kikomo.




Mansuli alifahamu kuwa alikuwa akifuatiliwa? Akajiuliza Frank Bambi. Hiyo ilitosha hakuona haja ya kuendelea kuhoji sana akachukua kilicho chake akaaga akiondoka huku mzee Mahamdu akimtania kuwa awe makini maana shughuli aendayo nayo nyumbani kwake si ndogo, Frank akacheka kwa utani.




*________*




Usafiri aupendao ulizidi kumkatishia mtaa huu na ule akichunguza hiki na kile huku kichwani mwake akijaribu kuumba matukio tofautitofauti kuendana na maelezo aliyoyaokota kutoka sehemu mbalimbali. Bado tukio la kushambuliwa kwa risasi la Mansuli Bingwa lilikuwa likijiumba kwenye ubongo wake taratibu.




'Alikuwa akishangaa upande wa nyuma yangu.....alikuwa mpole asiyeongea kitu tofauti na siku nyingine nilivyomzoea.....nilipogeuka kutazama anapotazama yeye, nikaona gari ndogo Toyota Vitara yenye namba za usajili U 768 AB.....!'




Aliwaza Frank akijaribu kuunda kitu kupitia maelezo ya Aliwatani Mahamdu. Hii sentensi ya alikuwa mpole tofauti na siku zote, ilimsumbua kidogo kichwani na kumfanya awe na wasiwasi huwenda Kamanda Mansuli Bingwa alikuwa akijua yupo kwenye usumbufu wa watu fulani. Alikijua kifo chake au alijua kuna watu wabaya walikuwa wakimkefyakefya kama si hivyo huwenda kwa uzoefu wake wa matukio hasa kwa kuwa muda mrefu kazini akilitumikia jeshi la polisi kwa vyeo mbalimbali huwenda alijua kuwa watu hao hawakuwa wema kwake...kwanini...? Kama alijua hivyo nini kimefanya asijiwekee ulinzi wa kutosha..? Ilikuwa sintofahamu kubwa sana hii. Kwanini akose raha? Akajiuliza zaidi huku pikipiki lake likiwa linaingia sehemu yenye maduka mengi akitokea katikati ya mji. Aliitazama saa yake ilikuwa tayari ni saa tano za asubuhi. Muda haukutaka mchezo kabisa katika kazi yake. Akatazama mbele akaona kuna duka moja kubwa la vyakula akapunguza mwendo na kutaka kusimama kabisa hapo pembezoni kidogo mwa barabara hata hivyo akapingana na amuzi hilo na kuamua kurudi tena barabarani, akasubiri gari moja ipite kisha aingie kwenye upande wake. Kuna jambo lilikuwa kichwani mwake na hakupenda kulaza damu. Kuna mtu alimkumbuka na alidhani angepata kitu chochote kutoka kwa mtu huyo kwani anafanya kazi sehemu husika hasa inayohusiana na hicho akipelelezacho. Akavuta klachi akapachika gia akaachia klachi kisha akavuta mafuta pikipiki likabadili muungurumo, dakika chache mbele akawa kwenye baa moja tulivu. Akaegesha pikipiki lake na kuvua kofia la usalama akaisawazisha miwani yake machoni na kutazama mandhari ya eneo hilo kabla ya kutoka juu ya hilo pikipiki. Baa ilikuwa tulivu kwa nje, hakukuwa na wingi wa watu akatazama bango lililopo juu ya mlango wa kuingilia kwenye baa hiyo akasoma maandishi yaliyosomeka; Utulivu Bar. Akateremka akapiga hatua ndogondogo hadi alipoufikia mlango wa kuingia ndani. Hakukuwa na watu wengi kwa majira hayo ya asubuhi, watu walihesabika. Akatoa simu yake ya mkononi na kupiga namba fulani baada ya kulitafuta faili la kuhifadhia namba au majina ya watu simuni humo. Simu ikaita kwa muito mrefu hadi ikakoma, hakusita kurudia, safari hii iliita kwa miito miwili ikapokelewa na mtu wa upande wa pili.




"Bambi!" Aliita hivyo mtu huyo wa upande wa pili wa simu.




"Habari yako ndugu yangu, uko kazini bila shaka maana nazisikia kelele zikirindima kwenye ngoma yangu ya sikio?" Akasema Frank Matiale Bambi.




"Ila kwa sasa natoka naelekea kupata chakula cha mchana." Akajibu wa upande wa pili wa simu.




"Ni saa tano na nusu sasa umewahi sana leo au ni ratiba mpya?"




"Hapana leo kazi ni nyingi sana ofisini hivyo inabidi kuufinya muda kwa ajili ya kupata chochote kitu kisha naweza kuutumia muda huu kwa muda wa ziada." Akajibu wa upande wa pili wa simu.




"Wapi unakwenda kupata chakula cha mchana?" Akauliza Frank .




"Napatia pale Baaghia Cafe Maduka mengi siendi mbali leo."




"Ok, tutakutana hapo imekuwa ni jambo jema sana kwani nilihitaji kuonana nawe leo." Frank akasema kisha akasikiliza upande wa pili, hakukuwa na jipya simu ikakatwa.










"Wapi unakwenda kupata chakula cha mchana?" Akauliza Frank .




"Napatia pale Baaghia Cafe Maduka mengi siendi mbali leo."




"Ok, tutakutana hapo imekuwa ni jambo jema sana kwani nilihitaji kuonana nawe leo." Frank akasema kisha akasikiliza upande wa pili, hakukuwa na jipya simu ikakatwa. Hakuingia tena kwenye ile baa akarudi lilipo pikipiki, akalipanda akaliwasha na kuliondoa hapo kwa mwendo wa taratibu kurudi Maduka mengi. Aliupima mwendo wake ili asiwe wa kwanza kufika Baaghia Cafe alitaka yule aliyempigia amtangulie na awe mwenyeji wake. Muda mfupi mbele alikuwa katika viunga vya Baaghia Cafe. Wakati anaegesha pikipiki lake akaiona gari moja nyeusi Noah ikiwa imeegeshwa kwenye maegesho ya magari akatabasamu na kukubaliana na hesabu zake. Hazikwenda maboya kwani mwenye gari hiyo ndiye aliyekuwa akimpigia simu. Akiwa anaingia kwenye mlango wa Cafe hiyo, kumbukumbu ya Toyota Vitara yenye namba U 768 AB. Ikamjia kichwani. Akauvuka mlango wa Cafe ile na kuyaangazia macho yake mule ndani, watu kadhaa waliziinamia sahani zao zilizosheheni misosi hakujali kama atachukua muda gani katika kuangaza macho yake, kwenye meza moja ya katikati akamuona mtu aliyekuwa akimuhitaji akiwa amesimamiwa na muhudumu wa eneo hilo akimpa maagizo. Frank akasogea hapo akavuta kiti cha Plastic akaketi.




"Tafadhali subiri!" Aliongea yule kijana ambaye ndiye hasa mtu aliyekuwa akimhitaji Frank kisha akamtaka muhudumu huyo kusikiliza shida ya mgeni wake, muhudumu akawa tayari kusikiliza.




"Nifanyie kahawa nyeusi ya moto tafadhali." Akaagiza Frank huku akiumba tabasamu usoni mwake ambalo lilipokelewa na huyo muhudumu kikazi zaidi.




"Kwanini iwe kahawa? Muda umekwenda sana huu zimesalia dakika tatu pekee kutimia saa sita kamili, agiza kitu kizito bwana." Akashangaa yule kijana mwenyeji wa Frank.




"Hapana swahiba usiweke shaka kwenye hili kuwa na amani mtimani. Nimejikalisha na shibe yangu hapa niliyoikwapua asubuhi kwenye kamgahawa fulani mjini, sitaki kukuacha mpweke katika ulaji, kahawa ingetosha." Akasema Frank huku akizidisha tabasamu.




"Sawa...mrembo, fanya vile ambavyo inatakiwa." Akasema yule kijana. Aliitwa Bokale Makasi, ni askari polisi mwenye cheo cha Sajini wa polisi afanyae kazi kwenye kituo cha polisi kati kituo ambacho mkuu wake wa kituo ndiye aliyeshambuliwa kwa risasi siku moja nyuma. Bokale Makasi alikuwa na ukaribu na Frank na kila mmoja alikuwa akijua jukumu la mwenzake vile ajuavyo yeye, Bokale alimjua Frank kama askari jeshi kutoke kikosi 42 huko Haika. Hii ilikuwa si kweli, hata hivyo Frank hakuwa akimjua huyu mtu kwa uchache tu kama yeye anavyofahamika bali alimjua kwa undani zaidi hivyo alikuwa na uhakika na kile akifanyacho.




Walianza mazungumzo yao kwa habari nyepesinyepesi hadi pale walipoingia kwenye mada husika na wakaliongelea hilo kama marafiki mara baada ya Frank Matiale Bambi kutoa pole kwa Bokale Makasi. Bokale hakusita kuipokea hata hivyo haikumzuia kueleza baadhi ya mambo ayahisiyo labda ndiyo yaliyohusika na kifo cha mkuu wake wa kazi.




"Kuna jambo lolote ambalo mkuu wako alikuwa akilionesha hivi karibuni ambalo huwenda halikuwa sawa?" Akauliza Frank Bambi mara baada ya kuupisha ukimya uliosababishwa na muhudumu aliyekuwa akihitimisha uletaji wa mahitaji aliyoagiziwa. Bokale Makasi akanyanyua kichwa juu na kulitazama feni lililokuwa likitenda kazi yake vema bila kuchoka ni kama aliyekuwa akisoma jambo kutokea hapo kwenye feni hilo.




"Alikuwa kawaida sana na mimi ndiye niliyekuwa karibu kila wakati maana ofisi yangu haiko mbali naye hivyo akienda akirudi huwa namuona. Ucheshi, maongezi na utani haukuwa na mapungufu kwa siku za karibuni hizi." Alijibu Bokale.




"Hakukuwa na mabadiliko umesema?" Akauliza kwa mtindo uleule ila huu ulikuwa ni wa kulazimisha kumbukumbu mgando kutoka kichwani mwa Bokale ziyeyuke angalau akumbuke kitu kutoka kwake. Bokale akaingia kwenye tafakuri nyingine ya muda mfupi. Akajiuliza kwanini swali hilo limejirudia na ilhali amelijibu. Alikuwa akiituma akili ya ziada itende jambo.




'Fikra iundwapo, fumbo hufumbuka ufikiriapo'.




Akakumbuka kitu ambacho kilijificha kichwani mwake Bokale Makasi ambacho hakungoja kiyeyuke, akainuka nacho.




"Siku mbili kabla ya kuvuma taarifa za kushambuliwa kwake kwa risasi," Frank Matiale akajiweka sawa. Bokale akaendelea.




".....alibadilika akawa si muongeaji wala msemaji wa mara kwa mara japo hali hii ilituhadaisha wengi kwa utani wake usiokoma na kicheko ambacho kwa hali halisi hakikuwa cha kwenye uvungu wa furaha ya kweli ya mtima wake. Nimepata picha sasa ulivyoniuliza swali hili kwa mkazo."




"Je, waweza kujua sababu ya mabadiliko haya?" Akauliza tena Frank safari hii akiongeza umakini mkubwa.




"Hapana sijui?" Akajibu Bokale kisha akainama na kupiga vijiko kadhaa vya chakula na kuushambulia mnofu wa paja la Bata mzinga akakiacha kinywa chake kitafune huku akiyatuma masikio yake kusikiliza vema. Frank baada ya kukitua kikombe cha kahawa mezani. Aliyazunguusha macho yake ndani ya mgahawa ule wote. Akaona watu walivyoongezeka kwa fujo akajua bila shaka huduma ya hapo imekuwa kivutio kikubwa sana kwa wateja. Macho yake yalimtazama kila mtu hata hivyo hakuona alichokuwa akikitazama kwenye macho ya watu hao zaidi ya sura zilizojaa bashasha na utamu wa chakula huku nyingine zikiwa na uhitaji wa chakula hicho kwa kuwasubiri wahudumu. Mafeni mane yaliyopandwa vema kwenye dari la eneo hilo yalitosha kuwafanya watu kuweza kujigamba na suti zao bila kuhisi wamevamia pasipo na hadhi yao.




"Je, hakuna watu waliyokuwa wakimfuata kamanda Mansuli Bingwa ofisini kwake na ninyi hamkuwafahamu?" Aliuliza Frank baada ya kutoka kuyatembeza macho yake mule ndani.




"Ni wengi!" Akajibu kirahisi Bokale Makasi huku akishindilia vijiko viwili vingine vya chakula kinywani akitazama saa yake. Frank akajua maana ya hiyo ni nini, alikuwa akiufukuza muda walau.




"Namaanisha wasioleweka?" Hapa Bokale akarudisha kijiko kwenye sahani na kumtazama Frank usoni kama achunguzae kitu kutoka kwenye sura shababi ya kijana huyo.




"Mbona unaniuliza mambo ambayo sikuwa nimefikiria kabla...., kuna watu walikuwa wakija kituoni kila siku ya juma tatu na hawa hawakuhitaji majadiliano na mtu yeyote au askari yeyote wao waliingia moja kwa moja kwenye ofisi ya mkuu wa kituo hata hivyo sikuwaza kuliingiza kwenye hisia zangu kuwa eti wanaingiliana na tukio hili ka mauaji yake. Ila mwisho wa yote yakawa mazoea. Yalikuwa ni mazoea yaliyojenga tabia shaka zikaondolewa machoni mwa kila askari kuna siku walikuwa wakitoka pamoja na mkuu wakiwa wanapishana kwa maongezi ya hapa na pale wakicheka. Na mkuu aliwahi kunadi kuwa hao walikuwa ni wafanyabiashara wenzake ambao walikuwa wakishirikiana katika ufanyaji biashara hivyo mara kwa mara hukutana na kuzungumza mengi. Tuliaminishwa hivyo na tukawa tumewazoea na hatukuleta shaka kwao. Hawa ndiyo waliyobadilisha hali ya mkuu....!"




"Kivipi?" Akadakia Frank Matiale na kuifanya sentesi ya Bokale Makasi kuogelea hewa.




"Siku tatu kabla ya mkuu kushambuliwa na risasi, hao watu walikuja hata hivyo hawakukaa sana wakaondoka. Walifululiza kwa siku mbili isipokuwa siku ya tukio la kuuawa kwa mkuu tu ndiyo hawakuja, walikuwa na suti muda wote idadi yao watatu hawakuzidi. Siku tatu za mwisho kama nilivyokueleza kuwa mkuu alikuwa kwenye hali ya kulazimisha kila jambo. Ucheshi, tabasamu hata utani, unadhani inaleta picha gani sasa hiyo?" Alieleza Bokale Makasi kwa vile alivyodhani.




"Walitumia usafiri gani kama unayo kumbukumbu?" Akatupa swali Frank.




"Gari waliyokuwa wakija nayo kila siku ni Toyota Vitara.....!" akajibu Bokale Makasi halafu akafikiri kwa kitambo kifupi.




"....nambaaa....aaah shiit...! Yea, namba za usajili ni U 768 AB, yaa, nimefanikiwa kuikumbuka." Akajibu Bokale makasi. Frank akarudisha kumbukumbu zake nyuma kwa kiwango cha juu sana, sasa amepata picha aitakayo, sasa alikuwa na uhakika wa asilimia miamoja na kitu kuwa hawa watu huwenda walikuwa wakimfuailia kamanda Mansuli Bingwa kwa muda mrefu sana hata hivyo akajiuliza walikuwa wakimfuatilia mtu huyo kwa sababu zipi?


Jibu lilikuwa ni uongo.




"Mnaweza kujua namna ya kuwapata hawa watu?" Akauliza Frank.


"Ni vigumu kwa kweli japo uchunguzi wa kina unafanyika ili watu hao waliohusika wapatikane." Alijibu Bokale Makasi.




"Kesi yake inapelelezwa na nani?" Akauliza baada ya kutafakari Frank.




"Kesi iko mikononi mwa Inspekta Mabula Babigale, faili la kesi hiyo ya mkuu wa kituo amekabidhiwa leo asubuhi na kaimu mkuu wa kituo, akahitaji ushirikiano mkubwa sana kutoka kwetu nilikuambia kuwa kuna kazi kubwa sana leo na miongoni mwake ni hiyo kwani kila aliyekaribu anatakiwa aaandae maelezo ya namna alivyoona au hisia zake juu ya jambo hili la kuogopesha na kushtusha. Nadhani umenifumbua sana kaka kwa hili naamini ripoti yangu ya maelezo itakuwa bora kuliko ya mtu yeyote yule na itaniweka kwenye nafasi hata ya kuwa askari mpelelezi mwandamizi wa kesi hii." Akasema Bokale Makasi akiwa na faraja iliyochomoza usoni mwake mithili jua la asubuhi.




"Nikutakie kazi njema kijana?" Akasema Frank huku akiona haina haja ya kuendelea kuhoji alitaka askari wafanye upelelezi wao kama walivyonadi na yeye afanye majukumu yake bila kuingiliana nao.




"Uliniitia hili tu kaka au kuna jingine?" Bokale akauliza kwa wasiwasi wa mshangao machoni mwake huku akijenga ulizo kuhusiana na iweje rafikie aombe kukutana naye kwa jambo hilo.




"Muda upo, nadhani tumekula muda mrefu baada ya kuibuka maswali ya kuhusiana na kifo hiki kilichomkuta kamanda Mansuli Bingwa. Nilichotaka kukizungumza nacho kinahitaji muda zaidi." Akasema Frank huku akiitazama saa yake. Muda ulikuwa umekimbia hivyo aliamini kuwa Bokale hakuwa na muda tena. Bokale naye akatazama saa yake.




"Muda hakuna kaka wacha niutumie huu uliyosalia nikaandae maelezo najua sitaumiza sana kichwa kwa kuwa umenisaidi kwa kiasi kikubwa sana." Alisema akiwa amenyanyuka tayari huku akitoa waleti yake na kutoa noti mbili moja ya shilingi elfu kumi na nyingine ya shilingi elfu tano akazitua mezani.




"Naona kahawa imepoa agiza nyingine kisha mkabidhi muhudumu pesa yake," akasema Bokale akiwa anayazungusha macho yake kushoto na kulia akafanikiwa kumuona muhudumu kisha akamuita akaaga na kuondoka, muhudumu yule alipofika alikutana na Frank Matiale.




"Kahawa yangu imepoa sana nami nahusudu ya moto, hebu niletee nyingine tafadhali kisha uje na bili yako." Akazungumza Frank akimtazama mwanadada huyo kwa tabasamu mwanana. Binti yule akaondoka. Macho yake yakamtazama muhudumu yule akamsifia muumbaji kwa kuweza kumtengeneza binti yule hadi kuwa mwenye mvuto wa kuwavuta wakora kwenye kuhitaji kumnasa. Mgahawa sasa ulikuwa umepoa sana kiasi cha kuweza kuukagua vizuri kwa macho. Ulikuwa na meza ambazo kwa wakati huo zote zilifanyiwa usafi, juu ya kila meza kulikuwa na vipambo fulani vya kumvutia mteja vikiwa vimesimikwa kwenye vikopo maalumu. Watu waliobakia walihesabika hata kwa macho tu bila kidole. Kahawa ilikuja akaanza kuinywa kwa utaratibu huku akichanganua hiki na kile kwa wakati huo. Alipomaliza alilipa na kurudishiwa chenchi iliyosalia akaondoka zake.






kulikuwa na vipambo fulani vya kumvutia mteja vikiwa vimesimikwa kwenye vikopo maalumu. Watu waliobakia walihesabika hata kwa macho tu bila kidole. Kahawa ilikuja akaanza kuinywa kwa utaratibu huku akichanganua hiki na kile kwa wakati huo. Alipomaliza alilipa na kurudishiwa chenchi iliyosalia akaondoka zake.




__________




Kwa kuwa ujio wao ndani ya jiji la Muavengero ulitambulika hawakuwa na wasiwasi kwani walishapewa uhakika wa kufuatwa asubuhi. Sembuyagi na Mabule walipoamka walijiandaa vya kutosha kisha wakatafuta mgahawa na kujipatia kifungua kinywa hata yalipotimu majira ya saa mbili na dakika ishirini asubuhi walikuwa wako tayari kwa ajili ya kuondoka. Muda mfupi mbele gari moja yenye rangi nyekundu iliegesha kwenye hoteli waliyofikia wakalifuata wakaingia kisha gari hilo likaondolewa kwa kasi kuelekea katikati ya jiji hilo. Safari yao iliishia kwenye jengo moja la ghorofa ambalo liliibeba ofisi moja miongoni mwa ofisi chache ndani ya nchi hiyo za usalama wa taifa. Waliingia ndani na kuongozwa moja kwa moja hadi kwenye ofisi husika.




Mbele yao kulikuwa na bwana mmoja aliye ndani ya suti iliyomkaa vizuri ya rangi nyeusi, akiwa na tai safi ya rangi nyekundu iliyolala vizuri kwenye shati jeupe safi. Alijaaliwa pua pana kiasi na mdomo mkubwa. Mbele ya bwana huyo kulikuwa na meza kubwa ya kunyurutika iliyojaa makabrasha mengi. Kulikuwapo na mafaili mbalimbali pia kulikuwapo na kopo maalimu la kuwekea kalamu, bendera ndogo yenye rangi nzuri ya Taifa hilo ilikuwa ikipepe juu ya meza ile kwa madaha makubwa. Bwana yule aliivua mawani yake ya kusomea kisha akaiweka kando akawatazama vijana wale wawili wakiwa wamejitwalia nafasi kwenye sofa kubwa la rangi ya samaawati kwa ajili ya wageni huku kukiwa na viti vingine vitano vilivyowekwa sehemu tofautitofauti macho yake makubwa meupe yakaonekana, hiyo yote ni baada ya kusalimiana kwa salamu za kijeshi kisha kuwaruhusu kuketi, tabasamu likawa ni sehemu moja wapo iliyomnyima muonekano wa kuvutia hakuwa na sura ya kuwafanya warembo kujisogeza kwake kuhitaji naye picha labda kwa mzaha. Aliitwa Domolangu Mabisu mkuu wa kitengo cha usalama wa Taifa Ungamo.




"Karibuni sana vijana?" Aliwakaribisha vijana wale bwana huyo. Mabule na Sembuyagi wakamtazama huku wakiupokea ukaribisho ule. Haikuwa na haja ya kupata maelezo mengi kutoka kwa vijana wale kabla yao kulishatangulia barua kutoka kwa mkuu wa kitengo cha usalama wa taifa Tanzania anayesimamia operesheni hiyo ambao wao waliipa jina la operesheni tafuta kuja kwenye ofisi hiyo. Maelezo ya barua hiyo yaliendana kabisa na operesheni ya kuwangamiza wanaondelea kuleta hofu ya uchafuzi wa amani nchini hapo ambayo ilipewa jina la operesheni safisha. Hivyo vijana hao kutokea Tanzania ambao walikuja kwa lengo la kuwatafuta madaktari wawili waliopotea au kutekwa kwa kipindi cha miaka 20 iliyopita, wakaunganishiwa faili jingine la 'operesheni Safisha Wachafuzi Wa Amani'. Walikabidhiwa faili hilo mara baada ya maelezo yaliyoshiba kuwa huwenda kwenye mpango uliyowaleta hapo nchini wahusika wa mpango huo ni wale wanaoendelea kuichafua amani ya nchi hiyo.




"Miaka 20 ni mingi sana mnataka kuniambia hao madaktari walipotea wakiwa na umri gani?" Aliuliza Domolangu Mabisu akiwa anacheka cheko la dhihaka kidogo. Sembuyagi akaona kama bwana huyo analeta dhihaka kwenye kazi ambayo taifa la Tanzania limekubali kuligharamia kwa kiasi kikubwa.




"Walikuwa si vijana si wazee." Alijibu Sembuyagi akiwa mkavu wa sura.




"Hamuoni kama mnaweza kujikuta mkihangaika kuitafuta mifupa?" Akauliza Mabisu akiwa ameweka utulivu na lile cheko akiwa amelificha mashavuni mwake.




"Litakuwa ni jambo la ushindi kwetu kama ikipatikana mifupa pia maana tulichokifuata ni watu wetu haitajalisha wapo kwenye hali ya namna gani." Alijibu Mabule huku akiwa kwenye utulivu mzito akimtazama bwana huyo. Mabisu akaurudisha mgongo wake nyuma ya kiti na kuwatazama hao vijana kwa macho huku ubongo wake ukiitazamia Tanzania na maamuzi haya ya aina yake. Vijana wake hakuwa na shaka nao hasa wakiwa kazini sifa ya nchi hiyo aliijua. Kilichompa ziada ya kufikiri zaidi ni kuhusu taifa kama taifa kujitoa kwa ajili ya watu wawili tu ni nchi gani inaweza? Hata kama ni wataalamu wa utabibu hata hivyo ilihitaji upendo uliyokithiri.


Si wa kulegalega.




"Nchi yenu ni ya kipekee sana na inaupendo na watu wake, nimeipenda bure nchi hiyo. Hamtakuwa wenyewe kwenye jambo hilo maana nahofia kuwaacha wenyewe halafu mkapambana na yanayotuhusu sisi hivyo mtakuwa na binti mmoja ambaye atakuwa pamoja nanyi." Aliongea Mabisu, Mabule akataka kupinga hata hivyo Sembuyagi Mpauko Haufi akamzuia asifanye jambo hilo. Hiyo ilikuwa na maana kuwa wapo tayari kushiriki kazi hiyo pamoja na huyo mtu. Walipokubali na kuridhika, Mabisu akanyanyua mkonga wa simu huku sura yake ikiwa haina tashwishi yoyote, hakuacha kumtazama Sembuyagi mara kwa mara. Alibofya vitufe kadhaa simuni kisha akaiweka sikioni.




"Namhitaji ndiyo," aliongea hivyo kisha akaishusha simu ile kwenye kibweta chake na kujiegamiza pale kitini akiwa kimya kabisa. Muda mfupi baadaye mlango ukabishwa akaruhusu na mtu aliyekuwa akibisha hodi akausukuma huo mlango na kujiingiza ndani. Alikuwa ni binti makini sana kwa urembo wake, sura iliumbika kifua kilichomoza mbele kwa mzigo wa haja wa matiti uliopata kuwekwa hapo kifuani, macho yalivutia kumtazama, kope za asili zilizolala, nyusi ndefu za asili zilizonyanyuka kidogo juu zilizidi kuongeza urembo wake na kuyapendezesha macho yake makubwa kiasi. Alikakamaa kwa heshima na kupiga saluti kwa mkuu wake wa kazi umbo lake matata likajichomoza vema. Alikuwa ametanuka kutokea kiunoni kwenda chini eneo la kwenye mapaja.




"Anaitwa Marietha ni mwana usalama kitengo hiki cha upelelezi hapa nchini. Hakuwekwa hapa kimakosa ni binti makini anayejua anafanya nini na ni mmoja wa wanausalama wanaoaminika hapa nchini. Tumaini langu ni kwamba atakuwa pamoja nanyi bega kwa bega hadi kufanikisha kazi yenu huwenda mtakapofanikisha kazi yenu nasi tutakuwa tumefanisha ya kwetu kwani naamini mbaya wenu ndiye mbaya wetu." Aliongea Domolangu Mabisu akimtambulisha mwanadada huyo. Marietha aliwasogelea vijana hao akawapa mkono na kwa heshima na taadhima wakasimama kuupokea mkono huo.


"Naitwa Mabule ni mwanausalama kitengo cha upelelezi nchini Tanzania," alijitambulisha akiupokea mkono wa binti huyo.




"Naitwa Sembuyagi Mpauko Haufi ni mwanausalama kutokea Tanzania," alijitambulisha pia kijana huyo huku akiupokea mkono wa Marietha. Ulikuwa mkono laini ambao haukumfanya adhani kama huyo angefiti kwenye shughuli hiyo.




"Nashukuru sana kuwafahamu nadhani tutafanya kile viongozi wetu wanavyotaka iwe tutakuwa pamoja kwenye kila jambo litakalotutaka kuwa pamoja hadi kufanikisha na nitakuwa chini yako pia kama kiongozi wangu." Aliongea Marietha akijishusha na kumpa uongozi kijana Sembuyagi mara baada ya kutoka kumtazama kwa tuo. Mabisu akatabasamu baada ya kukubaliana na utambulishanaji ule. Wakakaa kwenye nafasi na kupokea maelekezo muhimu na jinsi wanavyotakiwa kufanya kwani kama kiongozi alijua namna ya vijana wanavyotakiwa kufanya, akawapa yake kwa upande wake kisha mengine akawaachia wenyewe hakutaka kuwaingilia ni wenyewe wanajua watakavyoifanya kazi hiyo. Wakatakiwa kuondoka baada ya kupewa eneo ambalo wangekaa kwa ajili ya kuianza kazi yao, wakatoka pale wakiaga. Wakati Marietha anafika mlangoni aligeuka nyuma na kurudi baada ya kuusahau mkoba wake pale kwenye Sofa.




"Marietha, najua namna unavyotakiwa kufanya, najua unajua kwanini umeingia kwenye operesheni hii, fuata protokali za kiusalama najua umenielewa. Fanya kazi yako kama vile unayeishi na nyoka wa kufuga ambaye muda wowote unahisi ataota meno, usimuamini mtu." Aliongea Mabisu akiwa amesimama bila kutoka mbele ya kiti akimtazama Marietha usoni ambaye alikuwa ameukamatia mkoba wake.




"Hakuna kitakachoharibika mkuu kila kitu kitakuwa kwenye msitari usiwe na mashaka kabisa na mimi." Alijibu Marietha kisha akaondoka akiufungua mlango na kuufunga. Aliwakuta wenzake wakiwa wanalikaribia gari wakaliparamia na kumpa usumukani Marietha kwani yeye ndiye ambaye alitakiwa kuwaongoza hadi kwenye jengo walilokabidhiwa kwa ajili ya kwenda kuipanga mipango yao.




__________




Usiku sikupata nafasi ya kuikagua nyumba ambayo Luteni msataafu alinikabidhi na kuniambia kuwa ndiyo nitakayoanzia misheni yangu kwa awali, asubuhi ndipo nilipogundua kuwa nyumba hii haikuwa ndogo kwa ndani ukiingia ilikuwa ni nyumba kubwa yenye maficho ya siri sana. Ukiwa nje unaweza kudhani ni nyumba yenye vyumba vitatu sebule na maliwato la hasha! Ilikuwa ni nyumba ya aina yake. Kwanza ilibeba sebule kubwa ambayo ilikula eneo kubwa la kutosha vyumba viwili, chumba kimoja kiliwekwa mbali kidogo kutokea hapo sebuleni na kwenye chumba hiki kulikuwa na njia ya siri ya kulekea chini ya ardhi. Kabla ya kufika kote huko, kwanza nilianza na hii sebule. Ilipangwa kwa mpangilio wa kipekee sana meza kubwa ilikuwa katikati ikiambatana na viti vya kisasa vitatu huku pembeni mwa sebule hii kukiwa kumewekwa seti mbili za Sofa ambazo zilifanikiwa kwa kiasi kikubwa sana kuipendezesha sebule hii. Juu ya ile meza kulikuwa na vitabu viwili vikubwa, sikuzubaika sana na hapo sebuleni nilichokifanya ni kuanza kupekuwa hapa na pale kwani nilikumbuka maneno ya AKM kuwa nyumba hii ndiyo itakayonipa ufunguo wa kuianza kazi yangu au kama sio ufunguo basi ni silaha zitakazoweza kunisaidia kwenye misheni yangu nzima. Nilichakua rafu za vitabu na kusoma hiki na kile hadi nilipoweza kujiridhisha kwa nilichokifanya ingawa sikuwa nimepata kitu cha maana sana. Niliiacha hiyo sebule na kuifuata ile korido fupi ambayo ilinifikisha kilipo chumba kile ambacho nilipata kugusiwa kuwa ndicho chenye handaki la siri japo sikuwekwa wazi juu ya handaki hilo kindakindaki, nilipoingia hapo chumbani nikajua fika nilipoingia usiku sikuwa na kazi kubwa ya kuchunguza na pia sikuamua kulala humu chumbani na kuupitisha usiku pale sebuleni nilifanya hivyo kutokana na kuingia usiku mwingi ndani ya jengo hili hivyo nilivyoketi tu kochini usingizi ukanichota kizembe sana.










Niliiacha hiyo sebule na kuifuata ile korido fupi ambayo ilinifikisha kilipo chumba kile ambacho nilipata kugusiwa kuwa ndicho chenye handaki la siri japo sikuwekwa wazi juu ya handaki hilo kindakindaki, nilipoingia hapo chumbani nikajua fika nilipoingia usiku sikuwa na kazi kubwa ya kuchunguza na pia sikuamua kulala humu chumbani na kuupitisha usiku pale sebuleni nilifanya hivyo kutokana na kuingia usiku mwingi ndani ya jengo hili hivyo nilivyoketi tu kochini usingizi ukanichota kizembe sana.




Nilijilaumu mno kwa kubebwa na usingizi kama mfu ingawa sikuwa na namna zaidi ya kujipa utulivu nikizidi kuyatembeza macho yangu ndani mle. Chumba hiki kilikuwa na kitanda kimoja cha futi tano kwa sita, hakikuwa na kitu kingine cha kunifanya nikitazamie kwa macho ya kidadisi sana ila ukiachilia mbali kitanda, kulikuwa na kipande cha kapeti ya plastic yenye rangi nyekundu ikiwa na umbo la herufi 'T'. Ilitokea kilipoanzi kitanda kisha kikafika hadi ukutani. Nikashangaa kapeti ya aina hii, ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kuiona hii kapeti kwa namna ilivyotandikwa sakafuni. Nilipotazama vizuri niligundua kuwa pale katikati kulikuwa na mstari ambao ulionesha kuitenganisha hii kapeti, ulikuwa ni mstari wa rangi nyeusi. Niliitazama tena kwa makini ili kuona kama upo mstari mwingine sehemu nyingine ufananao na huo, sikuona. Nikaweka udadisi kwenye huu mstari nikausogelea na kuukagua kwa ukaribu. Haukuwa mstari kama ilivyo mistari mingine huu ulikuwa ni mgawanyisho wa hii kapeti hata hivyo iligawanyisha kiufundi sana. Nikavuta kipande kimoja cha kapeti ili kujiridhisha zaidi kuona kama kweli kapeti hii iligawanyishwa, hakikusogea kipande hata kimoja hii ilikuwa na maana kuwa kapeti hii ilishikizwa kabisa kwenye sakafu ya chumba hiki kwa gundi kali.




Haya yalikuwa ni maajabu....maajabu mengine ya kuajabisha.




Nikaachana na ile kapeti kisha nikaitazama sakafu ya hapo chumbani. Ilikuwa ni sakafu ya tarazo iliyopandwa kistadi. Kichwa kikaanza kuuma, nikanyanyuka na kujikalisha pale kitandani huku macho yangu yakiangaza zaidi. Juu ya dari kulikuwa na feni moja ndogo iliyopachikwa usawa wa kitanda, pembeni juu ya mlango wa kuingilia humo chumbani kulikuwa na taa ya mche. Nikatafuta swichi ambayo ilihusika kuendeshea vile vitu. Nilipo angalia mbele kwenye ukuta ambao ile kapeti au umbo la 'T' liliishia, niliona 'Double swich' ikiwa ukutani kwa juu usawa wa kifua changu nikisimama wima. Nikasimama kutokea pale kitandani na kupiga hatua ndogondogo kuisogelea ile swichi nikawasha moja baada ya nyingine nikagundua kuwa moja ilikuwa ikiendesha ile feni na nyingine ilikuwa ikiendesha ile taa.


Mbona makubwa!




Nikachoka na kurudi kitandani nikataka kukaa hata hivyo nikalipuuza wazo hilo huku kichwani kumbukumbu nyingine zikinijia.




'....Nenda kweye nyumba hiyo kwani hapo ndipo utakapoianzia safari yako...!'




Niliyakumbuka maneno ya AKM alipokuwa akinitaka kufika hapa. Bado nilikuwa na wazo la kuendelea kutafuta kabla sijashika kitu kingine. Nikageuka ghafula na kuitazama ile swichi pale ukutani, wazo fulani likanijia lilikuwa ni lazima linijie. Chumba kilikuwa kitupu na cheupe kiasi kwamba kama kungekuwa na kitu chenye kuonekana ni wazi ningekwisha kukiona mapema sana. Swichi ile ilikuwa na rangi nyeupe na miundo mingi ya swichi mbalimbali niliijua hivyo nikapanga kuichunguza hii swichi ili nione kama inafanana na zile ninazozifahamu. Kuna msukumoa ambao ulinilazimisha kufanya hivyo nao ni kwanini swichi moja ambayo kazi yake ilikuwa ni kuendesha mfumo wa taa, uendeshe taa na feni. Hii ikanipelekea niamini kuwa hapa kulikuwa na kazi ya ziada ambayo ilitumika na kujua hilo pia kulitaka mtu makini na mjuaji naye afanye kazi ya ziada kung'amua.


Aaama!




Niliisogelea tena ile swichi kisha nikaanza kuichunguza. Wazo langu halikuwa la kipumbavu hata kidogo. Katikati ya hii swichi yaani tukiacha ya kuwashia taa na ya kuwashia feni, kulikuwa na kinobu chenye rangi nyeupe pia mfano wa swichi yenyewe ilivyo. Ingekuwa ni vigumu kujua kitu hiki kama sikuwa nimesogea karibu nikiwa kwenye akili nyingine. Nilikiminya kile kinobu kikabonyea ndani, nikaanza kutazama kila kona hata hivyo jicho langu lilikomea kwenye sakafu ilipo ile kapeti na hiyo ni baada ya kushuhudia kipande cha kutokea kitandani kikipanda juu kisha kikasogea pembeni. Pale kilipotoka kulikuwa na mlango ambao ungemuwezesha mtu kupita. Nilisogea hadi kwenye huo mlango kisha nikachungulia, kulikuwa na ngazi ambayo ilikuwa ikielekea chini kabisa ya ardhi. Nilishuka bila kufikiria kitu chochote kile na kadiri nilivyokuwa nikipotelea huko ndani ndivyo giza lilivyokuwa kali zaidi. Nilifika huko chini hata hivyo kabla ya kuikanyaga sakafu ya huko chini, nilimulika kwanza kwa kurunzi yangu ya kijasusi ambayo aghalabu haikai mbali nami, sakafu haikuwa na shida, nilikanyaga na kumulika hapa na pale nikiwa sijapiga hatua hata moja, nikaona swichi nyingine ikiwa ukutani ambayo ilifanana na ile ya kule juu, nikaisogelea na kuiwasha kwanza taa ili kuleta mwangaza mule ndani. Uliibuka mwanga mkali uliyoingazia sehemu yote ya hapo, nikagusa kile kinobu cheupe nikaiona ile ngazi ikijikunja kwenye viungio vyake nikajua kile kipande cha sakafu kimerudi mahala pake. Niliwasha kiyoyozi ili kuweza kuiondoa hewa nzito ya huko chini na nikaanza kuchunguza kila kona ya eneo lile. Kulikuwa na vitu vingi sana kuna baadhi ya vyumba vidogo niliingia nikakutana na silaha za kutosha ambazo zilikuwa zimeshiba risasi huku vibebea risasi vikiwepo pia kulikuwapo na visu na silaha nyingine ndogondogo za kijasusi na zile za kijeshi. Kulikuwa na mavazi ya suti ambazo zilifichwa kwenye kabati la siri sana. Hapa kumbukumbu yangu ikanikumbusha maneno ya AKM kuwa nyumba hii ingeweza kunisaidi kuifanya kazi yangi vema, sikuona kingine alichokuwa akimaanisha zaidi ya hicho. Niliridhishwa na kila nilichokiona, sikuhitaji kuchukua kitu kwa sababu bado nilikuwa nikijitosheleza kwa kila kitu. Nilichukua baadhi ya vitu ambavyo vingekuwa kama uchunguzi kwangu. Nikataka kutoka hata hivyo kushotoni kwangu nikaona mlango nikaufungua hakukuwa na chumba bali hii huwenda ilikuwa ni njia maana niliona ngazi ndefu zilizokuwa zikielekea mahali. Nikataka kuzifutaka ngazi hizo ili kujua zimeelekea wapi hata hivyo nikapuuzia na kuufunga ule mlango kwa kuurudishia tu. Nilirudi pale nilipoanzia nikazima taa kisha nikabonyeza kile kinobu na kupanda kuelekea juu.




*_______*




Nilirudisha kila kitu kwenye nafasi yake nikatoka nje kabisa ya jengo lile nikachukua Peugeot 404 nikaingia mitaani. Njaa ilinisukuma kutoka mahali ninapoishi na kuelekea mahali ambako angalau ningepata chochote kitu cha kutia tumboni. Nilifika mjini nikakunja kona moja na kuingia kwenye barabara kubwa iliyokuwa ikienda kukutana na barabara ya Sami Ado, nikanyoosha na barabara hiyo kisha nilipofika mbele kidogo nikaiacha na kukunja kulia palipo na duka kubwa la vyakula nikapunguza mwendo huku nikiwa natazama mahali ambapo walau ningepata chakula. Nikiwa hapa macho yangu yalivutwa na kitu nisichokuwa nimekitarajia hata kidogo hii ikanifanya kuliondoa wazo la kupata chakula na kuanza kuliwekea umakini. Hii ilikuwa ni sehemu moja labda na muhimu pa kuanzia hivyo sikupenda kupuuzia. Gari niliyoiona kwenye soko kuu mjini nililiona tena hapo likiwa linatokea kwenye Super Market moja mtaa wa nyuma na kuja kuegeshwa kwenye lile duka la vyakula. Waliteremka watu wawili waliovalia suti za rangi nyeusi wakiwa wanatembea kwa mwendo wa haraka na kuingia kwenye lile duka la vyakula. Niliiondoa gari yangu hapo baada ya kupigiwa honi kwani gari yangu kwa namna fulani ilikuwa barabarani. Niliiondoa na kwenda kuegesha kando karibu na mgahawa mmoja uliyopo hapo karibu.




"Hawa watu ni akina nani na kwanini wako hapa? Je, kuna hatari nyingine ama?" Nilijinyuka maswali kadhaa huku nikiweka ubishi wa kujitoa garini. Nikiwa hapo nasubiri, niliwaona wakitoka na kuja nilipo. Nilitoa kamera yangu na kuwapiga picha kwa mbele bila wao kujua japo sikuwa nimezipata vizuri sura zao kwa namna ambavyo walikuwa wakitembea kisha nikatulia hivyo hivyo, hazikuwa picha nzuri sana kwa kuwa walikuwa kwa mbali kidogo na mahali nilipo. Baada ya kutoka kwenye lile duka la vyakula, niliwaona tena wakiingia kwenye ule mgahawa ambao nilitaka kuingia mimi kabla ya kuliondoa wazo la kula nilipowaona wao na kubadili eneo na kujiweka kwenye mgahawa mwingine wa upande wa pili wa barabara. Wazo la kula nililiweka kando kabisa na sikujua hata njaa ilijiweka wapi, akili yangu iliwaza kazi na si kitu kingine. Sikuchoka kusubiri na vilevile nilikuwa nikimuona mmoja kwa uchache kutokana na sehemu ambayo niliegesha gari yangu. Nikiwa naendelea na uvumilivu wangu. Nikawaona wakitoka kwa haraka huku wakiwa na wahaka machoni mwao. Nikachemka mwilini. Nikavuta dashi bodi na kuvuta pakiti ya sigara na kutoa sigara moja na kuipachika kwenye kingo zangu za midomo kabla ya kuirudisha ile pakiti mahala nilipoitoa. Nikatazama mbele ambapo niliwaona wale mabwana wakitazama walipokuwa wakitokea kwenye ule mgahawa. Niliona gari nyeusi Noah ikitoka kwenye kituo kimoja cha kujazia mafuta cha Oil Com na kuingia barabarani. Nikatazama wale mabwana nao nikawaona wakitoka pale walipokuwa wamesimama na kuifuata gari yao na kuingia kisha wakaiingiza barabarani nikajua huu ulikuwa ni mchezo wa hatari ulikuwa ikienda kutokea kwani hii Toyota Vitara yenye namba za usajili U 768 AB. Nilishaiweka kwenye alama zangu za hatari tangu nilipoiona pale kwenye tukio la mauaji ya kamanda Mansuli Bingwa. Nikasubiri magari mawili yanipite kisha nikaifuata hiyo barabara huku nikiliwahi gari kubwa la mizigo lisikae mbele yangu kwani lingeninyima nafasi ya kuona mbele. Niliitoa ile sigara kinywani mwangu na kuitupia juu ya Dashi bodi ikagaragara kwa masononeko, sikuwa mashuhuri katika uvutaji wa sigara hivyo sikuihurumia labda kwa vile sikuijua thamani yake. Akili yangu muda wote ilikuwa ikiwaza kuhusu wale jamaa waliyo ndani ya lile gari, ni wakina nani na kwanini wanauwa? Niliamini kwa asilimia kubwa kuwa ni wao ndiyo wauaji kwani niliwashuhudia wakitoka kufanya mauaji ya mtu ambaye nilikuja kumjua kuwa alikuwa ni mkuu wa kituo kikuu cha polisi mara baada ya kusikiliza taarifa ya habari kwa undani na maneno niliyoyapata kutoka kwa AKM.




Kwanini walimuua..? Jibu la swali hili sikulipata kwa undani labda kwa kuwa sijui kwanini. Kitendo cha leo kuwaona tena hapa wakimsubiria mwenye gari aina ya Noah ya rangi nyeusi, kikanipa mashaka na kuona haina budi kuwafuatilia.




Ile Toyota Vitatara iliingia kushoto na kuifuata barabara ya vumbi mara baada ya ile Noah kufanya hivyo, nikapunguza mwendo na kuwasha taa ya kuashiria kuwa naingia upande ule pia. Sasa nilikuwa nyuma ya magari yale, hakukuwa na gari nyingine ambayo ingeweza kunikinga. Akili yangu ikafanya kazi ya haraka sana mara baada ya kuona njia ndogo mbele iliyokuwa ikielekea kulia, nikaingia huko huku nikiziacha zile gari zikifukuzana na nilifanya hivyo nikiwa na makusudi maalumu kama huwenda nyuma yangu kungekuwa na gari nyingine ya kunifuatilia hivyo kufanya hivyo ilikuwa ni kupoteza lengo la mfuatiliaji. Sikuwa nimekwenda mbali sana na uoni wa macho yangu hata hivyo sikupoteza muda mwingi sana ghafula nikasikia mlipuko mkubwa sana wa risasi, haukuwa mmoja tu na wakaridhika bali ulijirudia zaidi ya mara tatu kisha kimya. Niliteremka na kuiacha gari yangu hapo kisha nikaelekea kuliko na tukio huku nikihakikisha hakuna mtu atakayenigundua kuwa mimi ni nani zaidi ya raia wa kawaida. Nilifika hapo na kuikuta gari ikiwa bado inatweta, kioo cha upande wa kushoto kikiwa hakifai kwa kuchanguliwa kwa risasi, chini kulikuwa na maganda ya risasi yapatayo mane, sikuhangaika nayo nilitazama ujio wa watu, nilipoona hakuna mtu anayesogea hapo nikafungua mlango na kuzama ndani. Lahaula!




Alikuwa ni mzee wa miaka kama 70 hivi kwa makadirio, alivaa shati la kitenge na suruali ya rangi ya ugoro aina ya Kodrai, chini akiwa amevaa 'Kubadhi'. Nilimpekuwa kwa haraka huku nikiyazunguusha macho yangu kutazama kama kungekuwa na mtu aliyekuwa karibu yangu. Hakuwepo mtu wa kunifanya nisite na watu walichelewa kufika labda kutokana na umbali wa makazi ya watu na hapo. Nilimkuta mzee huyu na kitambulisho cha uraia na kitambulisho cha kazi. Ambacho kilionesha kuwa hakuwa kazini kwa wakati huo. Alishastaafu. Alikuwa ni afisa usalama wa taifa. Mh! Niligumia baada ya kulishuhudia hili.






Hakuwepo mtu wa kunifanya nisite na watu walichelewa kufika labda kutokana na umbali wa makazi ya watu na hapo. Nilimkuta mzee huyu na kitambulisho cha uraia na kitambulisho cha kazi. Ambacho kilionesha kuwa hakuwa kazini kwa wakati huo. Alishastaafu. Alikuwa ni afisa usalama wa taifa. Mh! Niligumia baada ya kulishuhudia hili.




Inamaana wanaokufa ni watu wa usalama tu...? Nikajiuliza. Hata hivyo sikuwa na jibu la kujipa nilijihisi kama mlevi niliyemeza Afyuni. Nilizidi kumpeleleza huyu marehemu kwa kadiri nilivyoweza kwanza ilidibidi niwe na roho ngumu sana kuweza kufanya hivi maana kama ningelikuwa na roho ya ubua katu nisingejaribu hata kumsogelea. Kichwa chake kilikuwa kikiholomoka damu nzito yenye kuchangamana na ubongo wake baada ya risasi kadhaa kukifumua kichwa chake. Ilitisha sana hata hivyo ilikuwa imeshakuwa, mzee huyu alikutwa na ahadi ya kifo kwenye wakati mgumu sana. Sikufanya kazi kama ajizi kwani nilijua muda wowote hapo patakuwa hapafai na watu watajaa, nilichokipata kilinitosha hivyo niliufungua mlango wa gari na kutoka huku nikihakikisha hakuna alama niliyoiacha. Niliondoka nikirudi garini nikiwa na mawazo sana kuhusiana na watu hawa. Sikutaka kukurupuka na kufanya maamuzi ya haraka kwani niliogopa sana kuingilia kazi za watu wengine huku nikiacha kazi yangu iliyonifikisha nchini hapo. Niliingia ndani ya gari yangu kisha nikajiondoa taratibu hilo eneo.




___________




Mwanadada Marietha alikuwa akiiendesha gari taratibu kutokea mahali ambapo ndipo makazi yao yalipokuwa, akiwa anaingia mjini. Safari yao ilikuwa ikitakiwa kuhitimika kwenye ofisi moja mjini hapo kisha kunyoosha moja kwa moja hadi kituo kikuu cha polisi hapo mjini. Walitaka kuhakikisha wanaianza kazi yao kwa namna hiyo kwani hawakuwa na sababu maalumu ya kuendelea kusubiri ikiwa tayari walishapewa amri ya kuanza kazi. Wakati wanatoka kwenye nyumba hiyo na kuishika barabara ya Amakasi kisha kuchukua uelekeo wa kanisa la Anglikana, kabla hawajavuka barabara kuchukua uelekeo huo, Sembuyagi Mpauko Haufi akaomba gari hiyo iegeshwe pembeni, gari ikaegeshwa bila kuhoji. Jicho lake likawa makini sana kuyashangaa magari mawili yaliyokuwa yakiwapita kwa kasi sana, akatazama kupitia kioo cha nyuma cha gari akayaona magari yale yakiingia kushoto yakiwa dhahiri yakifukuzana.




"Umehisi nini kiongozi kwenye gari hizo?" Aliuliza Marietha akiwa anatazama kupitia kioo cha pembeni cha gari yake huku naye akiyaona magari hayo kwa mbali yakiifuata barabara hiyo nyoofu ya vumbi.




"Kuna hiyo Peugeot pia inaonekana kufuatana nao au?" Akauliza Mabule.




"Nina mashaka na zile mbili zinazofuatana, unaona hiyo Peugeot imeifuata barabara ya kuume? Hizi mbili bila shaka kutakuwa na namna." Akajibu Sembuyagi bado jicho lake likiwa kwenye kioo cha nyuma cha gari.




"Inabidi tuifuatilie kwa haraka sana huwenda ni watu wenye hila mbaya kwa wanayemfuatilia?" Akatoa wazo Marietha.




"Hapana, ngoja tuone kwanza itakavyokuwa." Akapinga Sembuyagi Mpauko. Mabishano yakaibuka kila mmoja akionesha muamko wake kwenye hilo. Kelele za mabishano yao ukilinganisha na umbali waliyopo sambamba na mpishano wa sauti za magari makubwa yapitayo kwenye barabara hiyo, ikawapelekea kutokusikia chochote kilichokuwa kikitukia huko. Mabishano yao yakamaliza dakika tatu nzima bila kujua wanachokifanya ni kupoteza wakati wao bure. Mwisho wa mabishano hayo ndipo wakafikia amuzi la pamoja kuwa sasa wanaweza kwenda huku Marietha akiona kuwa huwenda walishachelewa kufika kwenye tukio. Wakageuza gari na kuifuata barabara ile ambayo gari zile mbili zilifuatana, wakazidi kuifuata barabara ile ya vumbi kwa mwendo wa wastani kidogo, mbele yao wakaona kikundi kidogo cha watu kikiwa kimelizunguka gari lililokuwa likifukuziwa na lile jingine ambalo halikuwapo hapo.




"Tumechelewa!" Alihamaki Marietha huku akimakinika na hali ile. Fujo ndogo ya ule msongamano wa mashuhuda waliyojivika ushuhuda ikawalaki. Wakatoka garini na kulifuata lile gari.




"Amepasuliwa kichwa aisee! Na hii ndiyo iliyosababisha damu zitapakae kote huku kwenye kioo hiki cha mbele!" Sauti ya shuhuda mmoja ikasikika ikisema. Hii ikawapa mshawasha akina Sembuyagi Mpauko kuzidi kulisogelea na kulikagua kabla askari polisi hawaja vamia.




"Tupisheni kidogo tafadhali?" Aliomba Mabule akifungua mlango wa upande wa dereva na Mpauko akifungua ule wa kushotoni. Alikuwa ni mfu anayemwagika ubongo kwa suruba za risasi zilizompata kichwani. Macho yao ya umakini yakapeleka taarifa ubongoni kuwa hii ilikuwa ni zaidi ya hatari na wanazidi kuzembea kila kukicha. Kanuni ya kazi ilikuwa ikiwaonya kuanzia hapo. Kanuni iliwataka yasiongezeke mauaji ya namna hiyo mara tu baada ya kukabidhiwa kazi hiyo ya kusafisha. Hii ilikuwa ni kinyume cha kanuni hiyo kwani kila kitu kilikuwa kikienda sivyo ndivyo. Marietha alikuwa kimya sana huku kichwani mwake akiamini kwa asilimia kubwa kuwa walikuwa nao uwezo mkubwa sana wa kuweza kuzuia hilo lisifanyike kama yasingelitokea mabishano yale mafupi. Mabule aliingia ndani na kuanza kumpekua yule marehemu hawakukuta vitu vingine tofauti na vile ambavyo Catherine alivikuta. Kilikuwa ni kitambulisho cha kazi na vitu vingine vidogovidogo.




"Kwanini wanaua kwa namna hii na kifo hiki ni sawa kabisa na kifo kilichotoke Sokoni?" Akauliza Mabule baada ya kutoka kumpekua mtu huyo.




"Anaitwa nani?" Akauliza Sembuyagi.




"Kitambulisho chake kinamtambulisha kama Maviza Kavishe, aliwahi kuwa mwanausalama kitengo cha sheria na upelelezi," alijibu Mabule kwa mujibu wa kitambulisho kilivyosomeka. Sembuyagi akavuta ukimya kidogo na kumtazama yule marehemu kwa kina. Akiwa hajasema chochote, wakasikia ving'ora vya gari za polisi vikiwa vinakuja eneo hilo. Wakaamrishana waondoke kwani hawakutaka kazi yao iingiliane na polisi. Waliondoka kwa mwendo mrefu wakaja kusimama mbali sana na eneo walilokuwapo mwanzo.




"Kwanini tunazidi kuchelewa kuifikia hii hatari?" Akauliza Marietha akiwatazama mabwana wale wawili.




"Unadhani hatupendi kuwahi kufikia lengo?" Akauliza Sembuyagi badala ya kujibu alichoulizwa. Marietha akamtazama mtu mzima huyo kwa sekunde kadhaa kisha akayarudisha macho yake kwa kijana Mabule kabla ya kunyanyua tena kinywa chake.




"Nahofia kuzidiwa ujanja na tukashuhudia kifo kingine pasipo kumjua muuaji." Akatoa wasiwasi wake.




"Tulikuwa njiani kwenda kituo cha polisi na tukazuiwa na hili, kipi kinachokufanya uhisi kuwa tunakawia?" Akauliza tena Sembuyagi.




"Lengo ni kumfikia muuaji au kujua kwanini anaua, nadhani hili pia linaweza kutuleta kwenye hatua yetu ya kazi iliyotuleta hapa." Akajibu Mabule, Marietha akatikisa kichwa kuhusiana na hoja hiyo. Sembuyagi akawatazama kwa namna ya kupendeza kisha akaamrisha waelekee kituo cha polisi. Marietha akawasha gari na kutoweka eneo hilo. Dakika chache zilitosha kuwafikisha kilipo kituo cha polisi kikubwa wakatafuta maegesho na kuegesha gari yao. Kisha akateremka Sembuyagi Mpauko na Marietha wakaelekea ndani ya kituo hicho garini wakimuacha Mabule. Walipofika mapokezi walimkuta askari wa kike akiwa amejaa nyuma ya meza akiandika baadhi ya mambo jaladani.




"Habari yako afande?" Akasalimia Sembuyagi Mpauko kisha akauliza hitaji lake. Alitaka kuonana na askari aliyekabidhiwa kesi ya mauaji ya aliyekuwa mkuu wa kituo hicho. Dada yule akataka kuhoji zaidi kuhusiana na mtu huyo hata hivyo Sembuyagi akamuwahi kwa kutoa kitambulisho chake cha kazi na kukiweka mezani. Askari huyo wa kike akawatazama watu hao kwa zamu akajiridhisha kwa mtazamo wake wa hofu machoni kisha akawaambia waelekee kwenye ofisi ya kaimu mkuu wa kituo, ambaye ndiye aliyechukua nafasi ya muda baada ya mkuu wa kituo hicho kuuawa akawaelekeza mlango. Sembuyagi na Marietha wakaelekea walipoelekezwa huku jicho la afande wa mapokezi likiwasindikiza hadi pale walipopotelea ndani ya chumba cha mkuu huyo wa kituo wa muda.




Ofisini mule baada ya kukaribishwa walikutana na ofisi yenye muonekano wa kawaida sana na ile waliyoizoea kuiona, meza ya mkuu huyo wa kituo ilikuwa imebeba mafaili mengi yaliyofunuliwa na mengine kufunikwa. Huwenda mtu huyo aliyekabidhiwa ofisi alikuwa na mambo mengi sana ya kupitia kwenye kila faili ili kuona kitu ama vinginevyo. Aliwatazama wageni wake kishapo akawakaribisha waweze kutwaa nafasi.




"Asante sana mkuu, mimi naitwa Sembuyagi Mpauko Haufi!" Akajitambulisha.




"Na mimi naitwa Marietha Samson!" Naye akajitambulisha.




"Ni maafisa kutoka usalama wa taifa kitengo cha upelelezi hivyo tuko hapa kwa oda maalumu kutoka juu kuwa ni wajibu wetu kuchunguza kile kinachoendelea hapa nchini." Akajieleza zaidi Sembuyagi huku akiambatanisha maelezo hayo na kitambulisho chake cha kazi ambacho kilimtambulisha kama mwanausalama kutokea hapo nchini na si kama mtanzania. Mkuu huyo akawakodolea macho kama anayesoma kitu kutoka kwao.








"Ni maafisa kutoka usalama wa taifa kitengo cha upelelezi hivyo tuko hapa kwa oda maalumu kutoka juu kuwa ni wajibu wetu kuchunguza kile kinachoendelea hapa nchini." Akajieleza zaidi Sembuyagi huku akiambatanisha maelezo hayo na kitambulisho chake cha kazi ambacho kilimtambulisha kama mwanausalama kutokea hapo nchini na si kama mtanzania. Mkuu huyo akawakodolea macho kama anayesoma kitu kutoka kwao.




"Ndiyo, karibuni?" Hata hivyo aliwakaribisha zaidi.




"Tuko hapa kujua mwenendo mzima wa kifo cha aliyekuwa mkuu wa kituo hiki....!"




"Alivyouliwa au kwa namna gani?" Akawahi kuuliza mkuu huyo.




"Tukiwa na maana ya kutaka kujua maendeleo ya upelelezi wenu ulivyo na ulipofikia angalau kama mmepata picha yoyote kuhusiana na sababu za kifo chake?" Akauliza swali lililoshiba Marietha. Kaimu mkuu huyo akamtazama binti huyo kwa jozi kadhaa za sekunde kisha akasema.




"Vijana wangu niliyowapa kazi bado wapo kazini wanaendelea na uchunguzi hakuna kile ninachoweza kuwapa na kikawatosheleza maana kila kitu kiko kinaendelea kufanyiwa kazi muda huu." Akajibu kwa utulivu na kuwatazama kwa namna ya kuwasuta.




"Mkuu unajua tunahitaji nini, tujuavyo sisi utatuzi wa tatizo huanza lilipoanzia tatizo. Hivi ndivyo tuanzavyo kazi yetu sisi, hivyo ni matumaini yangu kuwa tutapata kitu kutoka kwako na hakuna sababu ya kuzunguuka. Vinginevyo useme tu kuwa unaweka kizingiti kuhusiana na uchunguzi wetu na kama unaweka kizingiti ni wazi fika kuwa unaizuia safari ya serikali hii katika operesheni yake safisha isifikie lengo. Nini au lipi kati ya hayo mawili unahusika nalo?" Akaongea kwa ukali kidogo Sembuyagi huku akimtazama mkuu huyo moja kwa moja usoni, hakukuwa na tashwishi yoyote usoni mwake. Kaimu mkuu wa kituo akameza funda la mate kujaribu kuitoa tashwishi usoni mwake. Alijawa na hofu tayari.




"Mnataka nini kutoka hapa?" Akauliza swali la kipuuzi ambalo lisingetarajiwa na yeyote yule kama angeuliza mtu mfano wake.




"Tumeshaeleza kwa mapana mkuu labda kama unakitu kingine hujajua." Akajibu Marietha. Mkuu huyo akavuta mtoto wa meza na kuchomoa karatasi mbili nyeupe zilizochapwa kisha akamkabidhi Marietha zile karatasi, Marietha alizifunua na kuzipitishia macho kwa sekunde kadhaa kisha akazipasi kwa Sembuyagi. Sembuyagi Mpauko naye alizipitia haraka haraka kisha akamtazama kaimu mkuu huyo wa nafasi iliyoachwa na marehemu kamanda Mansuli Bingwa. Alimuona kama bakanja tu kwa jinsi alivyokuwa akijizungusha kwenye kiti kile cha kiofisi kama bakuli tupu kisimani.




"Lipo zaidi ya haya maelezo?" Akauliza Sembuyagi Mpauko. Kaimu mkuu huyo akazunguusha kichwa chake kutoka kushoto kwenda kulia na kutoka kulia kwenda kushoto kwa mtindo wa haraka wa kurudia uwili. Sembuyagi Mpauko akanyanyuka na kufuatiwa na Marietha kisha wakatoka bila kushukuru. Walipofika garini walimkabidhi Mabule zile karatasi na kujiketisha sitini wakaondoka katika viunga hivyo vya kituo cha polisi.




__________




Wajuvi wa mambo wanasema mwanzo mzuri hukupa matokeo chanya. Frank Matiale alishajua nini cha kufanya na afanye nini kwa wakati gani. Mauaji ya Mansuli Bingwa yalishampa mwanga mara baada ya kupata maelezo kutoka kwa rafiki yake Bokale Makasi. Pamoja kuwa taarifa za kifo cha aliyewahi kuwa mwanausalama zilikita kichwani mwake kupitia vyombo vya habari hata hivyo hakutaka kukurupuka kwa kuamini muuaji alikuwa mmoja kulingana na mnyororo wa mauaji ulivyo. Aliijua gari iliyokuwa ikimtatiza na jinsi ya kuanza kuifuatilia hivyo hakuwa na shaka kwenye hilo. Giza lilikuwa tayari limekwisha kuingia hivyo akapanga kuituliza akili yake kwanza afikiri nini ambacho angeweza kufanya kwa wakati husika. Wakati huo Frank akijipa utulivu, ndani ya mji wa Makutano mashariki mwa jji la Muavengero, ndani ya jengo moja kubwa na tulivu tuna waona vijana wawili wakiwa na suti nyeusi wakiwa wamekaa kwenye sebule pana wakitazamana na meza kubwa ya mraba iliyowabebea chupa kadhaa za pombe kali huku chupa hizo zikiambatana na bilauri ndefu zilizo na nusu ya kimiminika hicho cha rangi ya mkojo wa mende. Walikuwa wawili tu pekee na hakukuwepo na mtu mwingine badala yao, waliendelea kupiga soga wenyewe taratibu huku wakiwa wanaendelea kumumunya kinywaji kile. Punde aliingia mtu mnene mwenye mwili uliyoshiba mazoezi ya kuzidi, mwenye suti ya rangi ya kijivu ilizomkaa vema. Alionekana kama aliyewehuka kidogo. Aliwatazama wale vijana wawili waliyokuwa wakiendelea kumumunya kinywaji kisha akawasabahi na kuwauliza.




"Bosi hajafika?"




"Bado, sisi ndiyo wafunguzi wa sebule hii nadhani." Akajibu kijana mmoja kati ya wale wawili aliyefahamika kwa jina la Welasoni. Bwana yule mwenye suti ya kijivu akanyanyua mkono wake na kutazama muda.




"Mwenzenu yuko wapi?" Akauliza yule mtu.


"Mkataba na yeye umekwisha kama ambavyo tulipewa taarifa na ameshalipwa chake kabisa na hivi tuongeavyo hayupo hapa nchini. Nadhani unajua kuwa hakutakiwa kujua chochote zaidi ya dili ya vifo vile viwili tu." Alijibu Welason.




"Ok, sawa!" Akajibu yule mtu mwenye suti ya kijivu kisha akatulia kidogo.




"Atakuwa amefika tayari." Alisema baada ya kutazama muda, hakukosea punde mlango wa kutoka varandani ulifunguliwa kisha mjongeo wa mtu ukasikika sambamba na mjongeo wa kitu kitumiacho magurudumu. Alikuja kutokea mtu mmoja aliyekuwa amevaa miwani ya giza, hakujali kama kwa wakati huo giza lilikuwa limeshachukua mamlaka yake. Mtu huyo alivaa suti za rangi ya kijivu pia lakini alikuwa akisukuma machela ambayo juu yake ilikuwa na mtu aliye katika vazi wavaalo wagonjwa maalumu la rangi ya kijani la moja kwa moja huku kukiwa na dripu ya dawa iliyokuwa ikitona matone taratibu kuingia mwilini mwa mtu huyo. Wote walionekana kama waliopata mzizimo fulani miilini mwao mithili ya watu waliyopigwa kidogo na mawaga maana mavazi yao yalionekana kuguswa na hali ya unyevunyevu kiasi. Mtu yule aliyekuwa akiisukuma machela ile aliiweka katika mkao mzuri kisha akabonyeza kitufe kimoja chini kidogo ya mahali kilipo kichwa cha mtu aliyeonekana kuwa ni mgonjwa kisha machela ile ikajitengeneza kama kiti ambacho kilimfanya yule mgonjwa kuonekana ameegama, sura ya mgonjwa yule ilikuwa imejikunja na alionekana kuwa ni mtu mzima kidogo. Kimya kifupi kikapita kabla ya mgonjwa yule ambaye alionekana kama aliyepooza viungo vya kuanzia kiunoni kwenda chini kujikohoza kidogo na kumtazama Amsuni Bhehe yule bwana mnene mwenye mwili mkakamavu wa mazoezi mwenye suti ya kijivu, hata hivyo alimudu kuongea na kufanya kila kitu japo kuna wakati alizubaa kwa mduwao kabisa hata kwa dakika nzima kishapo kuendelea tena kuongea. Baada ya mtazamo ule, Amsuni Bhehe alielewa nini alichotakiwa kukifanya kwa wakati huo, aliwageukia wale vijana na kuwaambia kuwa Bosi alitaka kusikia hatua waliyopiga na chochote kuhusiana na kazi hiyo.




"Mkuu, kazi inakwenda vizuri, hatua tuliyopiga inaridhisha na matumaini ya kuimaliza kazi hii yapo maana yamesalia machache ya kumalizia kabla ya kuwagusa walengwa." Alitoa maelezo yule kijana mwingine aliyefahamika kwa jina la Abdi Hussein.




"Si mnajua kuwa wanatakiwa watu watatu kwanza muhimu, mmoja ameshatangulia ambaye ni mkuu wa kituo cha poliai ambaye alijifanya kuijua kazi yake na kutuma vijana na kuleta shida kwa aliyekuwa bosi mkuu, tukiachana na yule kibaraka kutoka usalama wa taifa hesabu yetu inatuambia bado wawili hivyo mwanzo wenu ndiyo unatakiwa." Aliongea yule mwenye miwani ya giza.




"Hadi sasa tumefanikiwa kumuondoa duniani Mansuli Bingwa na Maviza Kavishe...!"




"Zaidi ya hapo ndiyo tunataka yaani mipango..!" Akawahi kuongea yule mtu mwenye miwani ya giza. Abdi Hussein aliendelea.




"Kwenye alama yetu hapa mikononi, tumebakiwa na Masuka Mvungi na aliyewahi kuwa Jaji mkuu bwana Kiago Mathias," yule mgonjwa akatikisa kichwa kuafiki kile kilichotolewa na vijana wale, akajivuta na kujiweka sawa pale kwenye machela yake iliyoundwa mfano wa kiti. Akasema.




"Ni siku mbili tu mnazo nataka kusikia kifo cha huyu mzee aliyewahi kuwa mwendesha mashtaka kabla ya kuwa mshauri wa karibu wa Rais lakini hapana....ninyi nataka leo mtekeleze kifo cha huyu aliyewahi kuwa Jaji kuhusu huyu mshauri wa Rais nitajua nani atahusika naye." Akamaliza kuongea kisha akatulia na kutazama mbele kwa karibia dakika nzima alikuwa ni kama mtu anayetaka kuanza kuvamiwa na ugonjwa wa kifafa, muda wote huo wengine walikuwa wametulia tuli huku wale vijana waliopewa maagizo wakinyanyuka na kuondoka eneo hilo. Punde alikaa sawa na kujifuta uso wake akawatazama wote kwa pamoja.




"Wameshaondoka?" Akauliza. Tally man yule kijana wa kuvaa miwani ya giza akajibu kuwa wamekwisha kuondoka. Huyu alikuwa ndiye mtu wa karibu na mlinzi mkuu wa bwana huyo mgonjwa ambaye aliitwa Malfrey Kobra.




"Maagizo?" Akauliza tena. Alikuwa akipoteza kumbukumbu zilizopita punde hasa linapotokea jambo lile la kuzubaa kwa muda kidogo kishapo hurudi akishakuwa amepoteza dakika kumi na tano, ishirini hadi thelathini.




"Kila kitu kiko sawa Bosi" alijibu Tally man. Malfrey Kobra akawatazama tena wale watu yaani mlinzi wake mkuu pamoja na Amsuni Bhehe kisha akanyanyua mkono ulibeba saa akaushusha na kutazama mlango wa kuingilia sebuleni hapo ulipo.




Ilikuwa imetimu saa tano usiku tayari, mlangoni pale alipotazama Malfrey Kobra au Bosi kama anavyotukuzwa, alikuwapo mtu mmoja aliyekuwa amevaa mavazi ya ajabu sana na hakuwa akionekana sura yake na si sura tu bali hata ngozi yake. Mwili wote ulifunikwa, alikuwa kama ninja. Alivaa mavazi meusi.






Ilikuwa imetimu saa tano usiku tayari, mlangoni pale alipotazama Malfrey Kobra au Bosi kama anavyotukuzwa, alikuwapo mtu mmoja aliyekuwa amevaa mavazi ya ajabu sana na hakuwa akionekana sura yake na si sura tu bali hata ngozi yake. Mwili wote ulifunikwa, alikuwa kama ninja. Alivaa mavazi meusi. Suruali nyeusi mfano wa Tracksuit, fulana ya kuvutika ambayo ilikuwa na vishikizo hafi chini ya kifua yenye mikono mirefu juu yake akiwa amevaa Jambakoti jeusi, mikononi alivaa soksi zilizoendana na vidole vyake kichwani alivaa kofia iliyokifunika kichwa chake na kumuacha macho pekee hata hivyo hiyo haikutosha akavaa na mawani ya giza huku chini akimalizia na buti kubwa la kijeshi. Mtu huyu alifanana kila kitu na yule aliyesababisha mauaji ya Dokta Gabriel Nyagile mjini Morogoro nchini Tanzania. Kwanini awe huku mtu huyu tena akiwa kwa watu waliyokuwa wakitekeleza mambo ya kinyama bila sababu ya kufanya hivyo kutokujulikana kwa wepesi ni nini hasa na ni nani mtu huyu?




"Karibu Black Scorpion?" Alikaribisha Malfrey Kobra akiachia kidogo tabasamu baada ya kumuona mtu huyo. Wote pale wakamshangaa huyo mtu kwani hawakuwa wakimjua kabla, Black Scorpion akaitika wito kwa sauti yake nzito kisha akasimama mbavuni mwa Malfrey.



ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog