Search This Blog

Thursday 29 December 2022

MPANGO WA NJE NI PIGO BUTU LA KIFO - 1

  

Simulizi : Mpango Wa Nje   Ni Pigo Butu La Kifo

Sehemu Ya Kwanza (1)

 


IMEANDIKWA NA : AHMED JIRIWA


********************************************************************************


Simulizi : Mpango Wa Nje - Ni Pigo Butu La Kifo 


Sehemu Ya Kwanza (1)




MWANZO WAKE.




Nilikuwa nikitembea kwa kujiamini sana sikujali hata kama nilikuwa nimechoka, mwendo wangu ulijaa madoido makubwa nilitembea kwa kuringa na kila mwanaume niliyepishana naye nilijua fika alivunja shingo kuniangalia mtoto nilivyojaaliwa na Mungu na kupewa maungo yasiyokera kutazama, mwanaume ungeshindwaje kuniangalia wakati nilikuwa na vigezo vyote vya kufanya uniangalie, nilijaaliwa sura hata kama si nzuri kupiliza hata hivyo ilitosha kunipa jeuri ya kujiona mrembo na kufikia kujikubali, kifua nilipewa mtoto wa kike hata kama si cha kubebea mizigo, kiuno si cha mikono kuishia katikati ninapokumbatiwa bali kufungana kabisa inapokutana. Kiuno chembamba chenye vigezo vyote vya kike, wenyewe wanaita kiuno cha Dondola. Nilipewa nyonga matata yenye kuhimili kuyabeba makalio yasiyo makubwa wala madogo, laini yenye kuleta mtetemeko wakati wa kuzitua hatua zangu chini. Nilikuwa jeuri siwatanii, jeuri wa kujua kuitumia ardhi wakati wa kutembea. Nilitembea kama inanidai.


Nilinata mtoto wa kike.


Hii si ile jeuri mnayodhani nyie ah, ah! Hii ilikuwa ni jeuri ya mikogo na hila, niliwaacha wanaume wenye tamaa ya kutamani vinavyoelea wavunje shingo nami wala sikujisumbua kuwashtua kwa kuwaangalia, nilichokifanya ni kuzidi kutumia mwendo wenye maumivu kwenye mioyo yao iliyojaa tamaa.


Niliwaumiza hasa.




Utanipatia wapi ukinitaka miye, mali ya watu nisiyejihisi tamaa kwa kutoka na mtu mwingine. Sikatai kuwa kuna muda huwa sina jinsi ilinibidi nijilainishe kwa mwanaume, nijinyongeshe na wakati mwingine niingie kwenye ngono na mwanaume huyo. Hivi nikivifanya huwa sifanyi makusudi bali nafanya kwa ajili ya kazi, tabia yangu ni kuwa sipendi kushindwa niwapo kazini natumia mbadala wa aina yoyote ile hadi nifanikishe nilichokipanga lakini si kwa kutafunwa tu bila mpangilio kama watoto wadogo watafunavyo Diamond Karanga.




Kagiza kalikuwa kanatanda hewani kama vile usiku ulikuwa ukiingia hata hivyo hakakunifanya nishindwe kuendelea kutumia miguu yangu. Halikuwa giza la kuukaribisha usiku lah! Lilikuwa ni wingu zito limetanda angani wingu ambalo lilikuwa likiashiria uwepo wa mvua wakati wowote na kama ingenyesha basi ilikuwa ni mvua kubwa sana. Baada ya muda mfupi mbele giza hilo likawa limeongezeka na kuchukua nafasi kubwa mno kwa harakaharaka kama ukiwa umekurupushwa usingizini ungeweza kulibatiza jina giza hili kuwa ni la saa tatu au hata nne usiku lakini wala! Ilikuwa yapata saa za katikati ya adhuhuri na alasiri kwa mujibu wa saa yangu ya mkononi ambayo mara nyingi nilipenda kuivaa. Ilikuwa saa nzuri sana ndogo kiasi yenye mikanda ya rangi ya dhahabu iliyokolea ilikuwa na kioo imara na mshale midogodogo huku mkanda wake ukiwa haujabana sana wala kulegea sana. Nilikuwa nimewahi sana kurudi nyumbani kwangu ninapoishi hii ilimaanisha kuwa nilicheza vizuri na akili yangu pale ilipoweka mashaka juu ya hali ya hewa hii isiyotabirika ya mkoa huu wa Morogoro. Sikuwa nimetumia usafiri binafsi siku hii nilitumia teksi makusudi kabisa kwani sikupenda kuminyana na usukani wa gari na kubadilisha badilisha gia mara kwa mara kwa ufupi ni kwamba sikupenda kujipa tabu kabisa siku hii. Nilipenda safari yangu niitembee ki-sister duu kabisa huku mara chache nikitembea kwa miguu kutoka sehemu moja hadi nyingine ili kuyapa shida macho ya vijana wasiopenda kupitwa na miondoko ya warembo aina yangu. Sipendi kujisifia sana na mara nyingi sipendi kujizungumzia kuhusiana na uzuri wangu ambao Mungu alinitunukia.




Sasa kwa majira haya, hatua zangu za taratibu nikazitupa kwa madaha makubwa nikilielekea lango la nyumbani kwangu. Ilikuwa ni nyumba ya wastani ambayo kwa mandhari yake ya nje yalizungukwa na maua ya hapa na pale ambayo yalipandwa kwa uzuri zaidi huku kukiwa na miti kadhaa ya kivuli ambayo haikuwa mikubwa sana na mtu aliyekuwa akiihudumia mandhari ya nyumba yangu upande huu wa nje, alijua kuupatia sana maana miti hiyo ilikuwa imekatwa kistadi sana kiasi kwamba huwezi kuchukizwa kuyatazama mazingira ya nyumba hii. Nililifikia lango la nyumba yangu nikalifungua kwa kupitisha ufunguo wangu kwenye makufuli mawili yalipotii amri ya mwenye nyumba na mmiliki wao nikausukuma mlango ambao nao haukuleta pingamizi lolote. Macho yangu yakakutana na mandhari ya eneo lile la ndani ambalo halikuwa na mambo mengi sana bali sakafu ya kisasa iliyopangwa vitofali vidogovidogo vya rangi ya aina moja, pembeni mwa baraza ya nyumba yangu kulikuwa na maua yaliyopandwa vizuri huku kukiwa na sehemu mbili za ile sakafu ambayo ilipandwa nyasi zilizokuwa zimestawi vizuri zilikuwa hazijakatwa kwa utaratibu ule niutakao na si kama sikuona lah! Nilitaka zikue kidogo ndipo zikatwe vizuri. Nilikuwa tayari nimeufikia mlango wa kuingilia ndani nao nikaufungua kwa mtindo uleule na kuusukuma. Kwanza nilikumbana na harufu ileile nipendayo kukutana nayo hasa ninapokuwa maeneo ya nyumbani kwangu ilikuwa ni harufu ya manukato ambayo niliipenda sana. Pili, nilikutana na mandhari nzuri ya sebule yangu yenye ukubwa wa wastani lakini uliopangiliwa vizuri kwani kulikuwa na seti moja ya sofa ya ngozi iliyo na rangi ya kahawia iliyotandikwa vitambaa vya rangi mchanganyiko na katikati ya ile seti ya sofa kukiwa na meza fupi na pana ya kioo iliyobeba vitu vichache vilivyoongeza uzuri wa sebule yangu, upande wa kushoto mwa ile sebule kulikuwa na Friji dogo ambalo lilikuwa na uwezo wa kupooza vizuri na kugandisha pia kulikuwa na kabati dogo lililotosha kunitunzia vyombo vyangu ambalo halikuleta kero pale sebuleni bali ni kuongeza uzuri. Niliweka hili kabati hapa kwa sababu sehemu ya jikoni ilijaa sana 'vikorokoro' vingi pia kulikuwa na runinga kubwa ukutani sambamba na muziki mkubwa aina ya Sonny yenye vispika vidogovidogo vilivyopachikwa kwenye pembe za dari pale sebuleni, dari lenye rangi nyeupe huku katikati ya lile dari kukiwa na taa kubwa ya kisasa iliyokuwa ikining'inia mfano wa urembo lakini ikiwa na yenye taa nyinginyingi za kuvutia ambazo huwaka kulingana na mwenyewe kupenda iwake kwa namna gani, pia kulikuwa na feni moja dogo lenye nguvu ambalo lilipandwa juu ya dari usawa wa ile seti ya Sofa ili kuleta hewa safi ya upepo pindi nikiwa hapo sebuleni. Niliipenda sana hii sebule na ili kuidhihirishia hilo kila nikirudi kutoka kwenye mihangaiko yangu ni lazima nipoteze sekunde kadhaa au dakika nzima kabisa nikiishangaa sebule hii kwa jinsi nilivyokuwa naitamani hata kuikumbatia kama ningepata wasaa huo. Nilijitupa kwenye moja ya Sofa lililopo pale sebuleni huku nikitoa sauti ya kuashiria uchovu wa mwili wangu nilichoka sana kutokana na matembezi yasiyo na kichwa wala miguu huku furaha kubwa niliyoipata ikiwa ni kukutana na marafiki zangu ambao niliwakumbuka sana maana kazi yangu inaniweka mbali sana na muda wa kukutana ama kuwatembelea marafiki hata ndugu na jamaa, muda wote nilikuwa katika mihangaiko inayozaliwa na kazi yangu ya kijasusi. Nilikuwa situlii utadhani Pantoni kivukoni. Sikujali, ni maisha niliyachangua na niliipenda kuliko kawaida kazi yangu hii na hata kama ingewekwa kwenye mafungu ya uchaguzi basi ningechagua ujasusi.




Niliyazunguusha macho yangu tena kwenye ile sebule huku nikiachia tabasamu tamu lenye mvuto kwa kuvutiwa nayo kila wakati. Nikiwa nazidi kuyazunguusha macho mule sebuleni nikakumbuka matembezi yangu ambayo yalihusishwa na marafiki zangu watatu Fatma, Rachel na Aurela, tulitembea sehemu mbalimbali kama Kilakala ambako tulizunguka kichochoro hiki na kile kisha safari yetu kuihitimisha Forest kwa dada yake Rachel ambako tulipoteza muda kidogo hapo kabla ya kuondoka na kuendele na matembezi yetu hadi pale tulipoachana na kila mmoja akaelekea nyumbani kwake. Yalikuwa ni matembezi yaliyoniacha nikiwa na furaha sana kwani katika kumbukumbu zangu sikuwa nakumbuka kama matembezi ya namna hii niliyafanya hivi karibuni. Hii ilikuwa ni siku ya pekee sana ambayo nitaikumbuka kila siku za maisha yangu, nilikuwa na haki ya kusema kuwa nitaikumbuka kwani sina hakika kama siku kama hii ingeweza kujirudia. Najua kuwa nilikuwa kwenye harakati za kuchukua likizo yangu ya mwezi mmoja mambo kama haya pengine yangejirudia nikiwa likizo.


Sidhani?


Nilikuwa na mambo mengi sana ya kufanya ambayo yaliuhitaji huu muda ambao ni mdogo sana hata kwa kuutazama hivyo burudani niliyoipata kwa matembezi ya pamoja na rafiki zangu sikuwa na uhakika kama yangeweza kujirudia.




Baada ya kujiridhisha na pumziko nililolipata hapo sebuleni kwangu nikajinyanyua kivivuvivu kisha nikaelekea kilipo chumba changu ambacho nacho kilikuwa na mlango, niliufungua kwa kutumbukiza ufunguo kwenye komeo lake kisha nikausukuma. Sikupenda kuacha mlango wazi hata kidogo kwani kufanya hivyo kwangu lilikuwa ni kosa kubwa mno nisilopenda kulifanya. Chumba changu kilikuwa kimekamilika hasa, kulikuwa na kitanda kikubwa cha futi sita kwa sita kilichotandikwa shuka safi lililonakshiwa rangi mbalimbali huku katikati ya shuka hilo kukiwa na picha kubwa ya Ua la kopa, upande wa kulia wa chumba hiki kulikuwa na 'Dreasing table' yenye kioo kirefu kilichotosha kujitazamia nikiwa nimesimama, upande wa kushoto kukiwa na kabati la nguo la kisasa kabisa ambalo lilivutia kulitazama. Kulikuwa na kapeti la manyoya chini lenye rangi mchanganyiko ambalo lilijaa sehemu yote ya mbele ya kitanda karibu na kona moja ya upande huu wa kulia kulikuwa na mlango wa kioo ambao ulirudishiwa, huu ulikuwa ni mlango wa bafu pamoja na choo/maliwato kwani chumba hiki kilikuwa kimejitosheleza kwa kila kitu. Sikupoteza muda nilizishusha nguo zangu kutoka mwili taratibu hadi pale niliposaliwa na nguo ya ndani pekee ndipo nilitwaa taulo langu na kuliviringisha mwilini mwangu kisha nikachukua uelekeo wa kuuelekea ule mlango wa maliwato. Huko nilioga vizuri kabisa na kumaliza huduma nyingine muhimu na kujirudisha tena pale chumbani. Niliifuata ile 'Dreasing table' na kukaribia kwenye kiti kilichopo mbele yake na kujiketisha.




Hakika nilikuwa mrembo sana sura yangu ilikuwa bado mbichi kabisa ambayo mbali na kujiremba pia nilivutia. Macho yangu makubwa kiasi ya kulegea yalifunikwa na kope ndefu kiasi za asili huku juu ya zile kope kukiwa na mstari mwembamba wa Nyusi uliotindwa vizuri kwa umbo la nusu mwezi, hii ilikuwa ni silaha tosha kwa wanaume wanaopenda warembo. Mashavu yangu hayakuwa na vishimo katikati yake lakini muumbaji alikuwa na makusudi yake kwani yalitosha kunipa jeuri ya kutabasamu nikiwa mbele ya mwanaume na nikamvutia ama kuzisumbua hisia zake za matamanio ya kufanya ngono na mimi. Nilipokuwa nikiendelea kujitazama pale kiooni nikashtushwa na muito wa simu yangu ulikuwa ni wimbo mzuri wa msanii mmoja maarufu wa kike hapa nchini, ilikuwa ikiita kwa sauti ya wastani hivyo kupelekea mashairi ya wimbo huo yasikike vizuri. Wimbo unaokwenda kwa jina la 'Ndi ndi ndi!' Wa mwanadada Lady jay dee. Nilimpenda sana mwanamuziki huyu na nilimpenda kwa mengi kwanza ni upambanaji wake kama mwanamke akishindana na dharau sambamba na changamoto nyingine nyingi ambazo zingeweza kuikatisha safari yake ya muziki kama inavyojionesha kwa wasanii wengine wa kike, pili ikiwa ni heshima aliyojiwekea kimuziki kiasi kupelekea kupata heshima kwa mashabiki wake wengi ambao sina shaka walikuwa ni wanawake wenye umri wa kati, juu na wachache wakiwa ni wanaume wanaoelewa nini maana ya heshima kwa mwanamke na tatu ni kujua kucheza na akili za mashabiki wake kujua wanataka nini na kwa wakati gani.


Alistahili heshima hakika.


Si kwa utashi wangu au upendo wangu kwa mwanamuziki huyu kiukweli alistahili sifa. Simu yangu ilikuwa bado inaita na si kama sikuona kuwa ilikuwa ikiita hata! Ila nilipenda kuusikiliza kidogo wimbo huo kisha niipokee. Nikasimama huku nikiwa nimeshikilia taulo kwa mbele kifuani mwangu lililoanza kulegea na kutaka kunitoka mwilini nikafika kitandani ambako ndiko niliiacha simu hiyo nikaichukua na kuitupia macho kiooni. Nikapatwa na mshtuko mdogo baada ya kuitazama namba iliyokuwa ikinipigia. Nilikuwa nikiifahamu nikajiuliza muda huu ambao ulikuwa ukikimbilia saa kumi za alasiri mpigaji alikuwa na shida gani. Si kama sikupenda anipigie hata! Hakuwa na mipaka kwangu hasa aamuwapo kunipigia hata hivyo moyo wangu ulihisi jambo. Si mtu wa kunipigia simu mara kwa mara hasa kwenye namba hii ambayo ilikuwa haitumiwi sana na ofisi. Nilijikuta nikikaa kitandani huku nikiubana kabisa mkono uliokamata taulo kifuani ili kuongeza uimara wa ulinzi wa kifua changu kilichobeba matiti imara na yenye mvuto mkubwa huku yakiwa na chuchu imara zenye rangi nyeusi zisizotetereka.


Kuna usalama kweli...? Mbona sikuwa na taarifa kuwa...kuwa atapiga simu...? Niliwaza nikijiuliza maswali mfululizo hata hivyo sikuwa na namna zaidi ya kuipokea.










Hakuwa na mipaka kwangu hasa aamuwapo kunipigia hata hivyo moyo wangu ulihisi jambo. Si mtu wa kunipigia simu mara kwa mara hasa kwenye namba hii ambayo ilikuwa haitumiwi sana na ofisi. Nilijikuta nikikaa kitandani huku nikiubana kabisa mkono uliokamata taulo kifuani ili kuongeza uimara wa ulinzi wa kifua changu kilichobeba matiti imara na yenye mvuto mkubwa huku yakiwa na chuchu imara zenye rangi nyeusi zisizotetereka.


Kuna usalama kweli...? Mbona sikuwa na taarifa kuwa...kuwa atapiga simu...? Niliwaza nikijiuliza maswali mfululizo hata hivyo sikuwa na namna zaidi ya kuipokea.


Nikaipokea simu ile na kuiweka sikioni.




"Haloo mkuu....!" Nilianzisha maongezi baada ya kuipokea na kuiweka sikioni kisha nikatega sikio kusikiliza kabla ya kuongea tena.


"Muda huu....?" Nikauliza nikiwa na macho yaliyo na alama za mshangao wa kutokuelewa nikasikiliza tena lakini nikajikuta nimeishusha simu yangu na kuiweka kitandani baada ya kujibiwa kuwa ni muda huo nilitakiwa kwenye wito na simu ya upande wa pili kukatwa. Akili yangu ilianza kupata wasiwasi na kuuliza kunani....? Mwili niliuhisi ukianza kutoa jasho na ilhali nimetoka hivyo punde kuoga. Nikapata mashaka na kujishangaa kwanini nimekuwa hivyo. Nilipokumbuka kuwa ulikuwa ni wito wa haraka na aliyeniita ni mtu ninayemuheshimu sana na kiongozi wangu wa pekee katika kitengo hatari na cha siri cha kijasusi ambacho kilikuwa kikipambana na hatari za kijasusi ama uhalifu wa kuleta hofu nchini, nikairudisha akili yangu katika utulivu na kujirudisha tena pale kwenye eneo langu la kujiremba na kuifanya kazi hiyo kwa haraka kubwa.




__________




Naitwa Catherine wa Catherine au waweza kuniita Catherine tu inatosha, ningependa unitambue kwa jina hili lakini pia si vibaya ukiniita 'Green Bird' jina pekee nililopewa na rafiki yangu Aurola. Alinipa jina hili kutokana na uadimu wangu wa kutokuonekana hovyo mitaani nami nikalipenda na kulipa maana kubwa zaidi kwenye maisha yangu. Mimi ni jasusi....ni jasusi hatari sana na namba mbili wa kitengo ninachofanyia kazi ambacho kazi yake kubwa ni kupambana na matizo makubwa ya kijasusi ndani na nje ya nchi. Jasusi asiye na mipaka. Hii ndiyo sababu pekee inayoniweka mbali na shughuli nyingine za kawaida hivyo kuwa adimu kupitiliza.


Kwanini nisiwe ndege wa kijani?


Sikuingia kwenye kitengo hiki kimakosa nimefuzu mafunzo makali ya kijeshi na kijasusi kwenye mashirika makubwa duniani kabla ya kuwa chini ya kitengo hiki ambacho kilianzishwa maalumu baada ya kuona kuna umuhimu mkubwa wa kufanya hivi hasa ni mara baada ya serikali kujua kuwa kuna mambo ya hatari yaliyokuwa yakichimbuliwa chini kwa chini huku hatari yake ikiwa ni tishio kwa taifa. Ni mtu makini sana na hatari kama ukiingia kwenye kumi na nane zangu, niko nyuma ya kijana hatari na makini anayefahamika kwa jina la Rajab Omair Isihaq mwenye 'Code name' Roi. Huyu kwa sasa hayupo nchini amekwenda nchini Uganda kwa kazi maalumu. Naipenda sana kazi yangu na niko radhi kufanya lolote na popote ilimradi tu amri ya kufanya hivyo iwe imetoka kwa mkuu wangu.




Nilimaliza kujipodoa nikajitazama kwenye kioo katika namna ya kujichunguza kama nilikuwa nimekamilika. Uzuri wangu ni kama uliongezeka mara mbili nywele zangu nilizozifunga kwa nyuma na kuonekana kama mkia wa Farasi zilinipa mvuto mkubwa, nilijua kuzijulia kwani zilimeremeta sana kwa mafuta maalumu ya nywele niyapendayo ambayo si ya gharama kubwa lakini ni yenye kuziacha nywele zangu katika mvuto mkubwa, rangi ya mdomo nyekundu pamoja na wanja nilioupaka kistaarabu vimeongeza thamani kubwa ya urembo wangu nilipendeza sana kiasi cha kuona vile nitakavyoweza kuwavunja shingo watu mtaani. Nilivaa suti yangu matata sana ya rangi ya kijivu ambayo huwa naipenda sana kwasababu huwa inaniweka katika muonekano wa kipekee sana nilitabasamu baada ya kujitazama pale kiooni kisha nikaukumbuka wito wa mkuu wangu wa kazi. Sikupoteza muda nilichukua funguo zangu za gari na muda mfupi nikawa nje kwenye maegesho yangu ya magari nikafungua mlango wa gari yangu aina ya Toyota Corolla nikajiweka sawa kitini na kuliwasha kabla ya kuirudisha nyuma na kuiondoa kwa mwendo wa taratibu kuingia barabarani ambako niliongeza mwendo. Muda mfupi mbele nilikuwa Kituo kidogo cha mabasi cha Masika nikanyoosha mbele na kuipitia Benki ya CRDB Masika kisha nikachukua barabara ya Makongoro iliyonifikisha kwenye makutano ya barabara ya Madaraka nikanyoosha barabara hiyo ya Uhuru nikiiacha barabara hiyo ya Madaraka hadi mbele kidogo nikakunja kulia na kuongeza mwendo kidogo wa gari yangu huku nikinyanyua mkono na kuitazama saa yangu ya mkononi. Muda ulikuwa ukinitupa mkono sana na sikutaka kuchelewa kabisa. Niliiacha hoteli ya Mt. Uruguru na kwenda mbele zaidi kabla ya kukunja tena kulia nikaifuata barabara hiyo kwa mwendo mfupi nikaingia kushoto nikaendesha. Muziki laini uliokuwa ukipiga kutoka kwenye spika za Redio yangu ulikuwa ukinipa burudani ile niitakayo kiasi kwamba muda mwingine nilikuwa nikiifuatilia sauti ya muimbaji. Ilinipunguzia mawazo kwa kiasi fulani kwani sikuwa nikikumbuka mambo ya ajabu ajabu akili yangu kwa muda huo ilitekwa na mawimbi hayo ya sauti iliyonaksiwa vizuri kwa kinanda kilichopigwa kiufundi, mawimbi hayo yaliibeba akili yangu na kuipeleka kwenye sayari ya mbali kabisa. Mji huu wa Morogoro haukuwa na pilikapilika nyingi sana kwenye barabara zake hivyo kunifanya kuwa huru sana nikiwa naendesha gari, watu wachache waliokuwa wakitembea kwa miguu kando ya barabara na magari machache na pikipiki nilizokuwa nikipishana nazo ziliifanya hali ya utulivu uwe wa kueleweka zaidi. Macho yangu yaliyokuwa nyuma ya miwani yangu ya kike nyeusi hayakuacha kutazama nje kila pande nikiyashangaa mandhari ya maeneo mbalimbali. Nilizidi kuendesha gari hadi Duka la dawa la Chowe nikanyoosha na barabara hiyo hadi Rombo White Bar. Hapa nikatafuta maegesho ya magari nzuri ili niweze kuegesha gari yangu hakukuwa na magari mengi. Kulikuwa na magari matatu ambayo hayakuwa yameegeshwa karibu karibu hivyo kulikuwa na nafasi nzuri ya mimi kuegesha la kwangu, nikaliingiza gari langu katikati ya magari mawili kisha kabla ya kushuka nikayatembeza macho yangu nikiitazama baa ile kuanzia ndani kupitia kwenye kuta fupi za baa hiyo hadi mlangoni ambako kulikuwa na kijana mmoja aliyekuwa akiingia hapo ndani mara baada ya kufika hapo punde na pikipiki yake. Sikuona jambo jingine la kunivutia kulitazama hivyo nikateremka na kuufunga vizuri mlango kisha nikatia mfukoni funguo zangu za gari na kuanza kupiga hatua ndogondogo nikiifuata baa ile kabla sijaifikia, nikakunja kulia na kutembea ubavuni mwa ukuta ule mdogo wa baa ile hadi nilipoiacha kwa hatua kama kumi na tano. Nikazidi kunyoosha mbele na kukatiza kwenye barabara ile iliyokuwa ikitokea Mt. Uluguru nikanyoosha mbele zaidi nikizidi kuzitupa hatua zangu taratibu nikafika kwenye jumba moja kubwa ambalo lilikuwa tulivu sana kwa majira hayo. Sikupoteza muda nikaingia ndani ya jumba hilo kwa kuufuata mlango ambao haukunipa shida sana kuusukuma nikapokewa na korido ndefu na nyembamba ambayo pembeni mwake ilikingwa na kuta zenye rangi ya maziwa iliyofifia juu huku chini zikiwa zimepakwa zangi nyeusi iliyong'ara. Niliifuata korido hiyo huku ukimya ukiwa bado mkubwa kiasi kwamba mjongeo wa hatua zangu za kike zenye ukakamavu zikawa ndizo pekee zinazosikika kutokana na kuvaa viatu vyenye visigino virefu. Niliifuata korido hiyo hadi mbele ambako nilikutana na njia mbili moja ilikuwa ikielekea kulia na nyingine kushoto, nikaichukua ya kushoto na kuifuata hata hivyo haikunifikisha mbali. Mbele kidogo nikakutana na mlango wa lifti ambao niliufungua kwa kubonyeza kitufe cha kuuruhusu mlango huo ufunguke na kuingia ndani mlango ule ukajifunga nyuma yangu nikabonyeza vitufe kadhaa ukutani kisha nikatulia. Lifti hiyo ilinichukua hapo na kunipeleka ghorofa ya pili mlango ulipojifungua nikatoka na kuifuata korido ndogo iliyokuwa imetazamana na milango minne, miwili kushotoni kwangu na miwili kuliani kwangu. Nikatembea kwa hatua kadhaa kabla ya kukutana na mlango mmoja ambao haukuwa miongoni mwa ile milango minne. Nikagonga mara moja kisha nikatulia kwa sekunde tano nikausukuma na kuingia ndani. Macho yangu yalikaribishwa na mandhari nzuri ya ofisi hiyo. Kulikuwa na kapeti ngumu ya rangi ya mawingumawingu iliyochorwa maumbo mbalimbali huku kukiwa na meza kubwa ya mbao ngumu yenye umbo la nusu duara, nyuma ya meza hiyo alikuwako mzee mwenye kipara kilichokuwa kikiwaka sana mithili kilichopakwa mafuta. Mzee mkakamavu aliyepitia vyeo mbalimbali vya jeshi la Tanzania mwisho akakabidhiwa kitengo hiki hatari kabisa cha kijasusi Luteni. Nikayahamisha macho yangu toka kwa mzee huyo na kutazama juu ya ile meza ambako kulikuwa na vitu vingi vya kiofisi vilivyopangwa uzuri kabisa. Kulikuwa na glasi fupi ya kioo kigumu iliyojaa kalamu mbalimbali zenye rangi tofauti kama nyekundu, nyeusi, buluu na zenye rangi mchanganyiko, kulikuwa na mafaili matatu yaliyobebana kulikuwa na kikombe kipana cha udongo maalumu kwa kutunzia majivu na vipisi vya sigara zilizokwisha tumika, kulikuwa na tarakilishi mbili moja ikiwa imefunikwa na nyingine ikiwa umefunuliwa ikitazamana na mzee huyo, kulikuwa na runinga kubwa ukutani. Nilizidi kuyatembeza macho yangu kama vile ni mara yangu ya kwanza kufika ndani ya ofisi hii.




Kama zilivyo ofisi nyingi za kiserikali au hata binafsi, kulikuwa na kitofali cha chuma chenye rangi nyeusi ambacho kilibeba bendera ya taifa upande wa kulia wa ile meza ukutani kulikuwa na rafu kubwa ya vitabu na mafaili mbalimbali huku juu ya rafu ile kukiwa na boksi dogo lililofungwa kwa gundi ya karatasi huku juu ya lile boksi ukutani kukiwa na kalenda kubwa yenye picha. Upande wa kushoto kulikuwa na makochi mane makubwa ya rangi nyeusi kwa ajili ya vikao mbalimbali nyeti ama shughuli nyingine za kiofisi.




"Karibu uketi Catherine!" Sauti ya yule mzee aliye nyuma ya meza yake ya ofisi ilinigutusha, nilipomtazama usoni niligundua kuwa alikuwa akinitazama muda mrefu tangu kunusisha pua yangu mule ofisini huku akiwa katika tabasamu hafifu usoni mwake alikuwa akiupuliza moshi mwembamba wa sigara kutokea kinywani mwake. Nikakitazama kiti kilichopo mbele ya ile meza kilichokuwa kikitazama na mzee yule, nikatabasamu ikiwa ni kama kurudisha salamu kwa mzee huyo. Nampenda sana huyu mtu ni mpole makini sana japo sikuwa nimemzoe vya kutosha ila nilimtambua kwa kiasi kikubwa, jina lake ni Daniel Matia Okale au unaweza kumuita mwalimu Dao kama jina lake la kificho. Hana muda mrefu tangu achukue uongozi kwenye ofisi hii yapata miaka miwili hivi na ushei, alichukua nafasi hii mara baada ya aliyekuwa mkuu wa kitengo hiki cha ujasusi Hussein Babu kusemekana kupoteza maisha japo bado uchunguzi wa jambo hilo la kuhakikisha kama kweli alipoteza maisha ama lah! ukiwa unaendelea. Sijui sababu ya kuniita ndani ya ofisi hii ndogo ya NISA lakini huwenda kulikuwa kuna jambo lilikuwa mbele yangu sinashaka maana hii haikuwa kawaida yake kabisa.


Nilimuamkua kwa heshima za kijeshi kwa kupiga saluti huku nikionesha nidhamu ya hali ya juu mbele ya kiongozi wangu huyo kwa ghafula nikiufukuza utani wa kawaida, alipokea salamu yangu ile ya kijeshi kwa tabadamu lake hafifu kisha nikavuta kiti kile kilichokuwa kikitazamana naye na kuketi nikiweka utulivu mkubwa huku tabasamu langu likiweka makazi usoni mwangu. Akanitazama kwa makini na utulivu wa hali ya juu.


Akaweka tuo katika mtazamo wake kidogo kisha akaipigapiga sigara yake kwenye kingo za kile kikombe kizito na kipana cha majivu akaipachika sigara ile kwenye kingo za midomo yake na kuivuta, akatoa moshi mwingi nje na kunitazama kwa makini.


"Nina wiki sasa sijapata kukuona kama huishi ndani ya mji huu, nilijua tayari umekwisha kutimka nje ya hapa?" Akaniuliza huku akiiweka tena sigara yake kwenye kingo za midomo yake akiivuta huku akinitazama kwa utulivu na tabasamu jepesi. Nilijua alikuwa akinitania maana nisingeweza kuondoka pasipo utaratibu wa kikazi. Nikamtazama huku nikitafuta namna ya kumjibu kama alivyoniuliza.


"Niko kwenye maandalizi ya kuchukua likizo yangu mkuu?" Nilimwambia huku nikimtazama usoni. Nilimuona akigeuka na kutazama upande ule ulio na Rafu ya vitabu na mafaili mbalimbali akashusha pumzi kwa nguvu na kutulia kwa sekunde kadhaa akiwa kama anaye fikiria jambo zito. Akanitazama akiwa amepoteza furaha ile ambayo nilimkuta nayo awali wakati naingia humo ofisini nikajua lipo jambo.


"Nasikitika kuwa likizo yako haipo," akaweka koma huku akinitazama kinyonge nilipatwa na mshituko mdogo na kuvurugika kwa mawazo yangu ya kuhusiana na yote niliyoyapanga nikiwa likizo. Hili nililitarajia ingawa sikuwa nikiomba iwe hivyo kwa namna hii ilivyokuwa hata hivyo nikawa nauhamisha mshtuko wangu na kuupeleka mbali nami taratibu. Lilikuwa ni jambo la ghafula sana na lililonipotezea nguvu kwa muda mfupi.


"Likizo yako imesogezwa mbele....!"


"Kwanini mkuu?" Nilimuuliza kwa kihoro nikimtazama kwa makini usoni hata hivyo alikuwa kwenye utulivu wa hali ya juu sana akaipachika sigara yake kwenye midomo yake kama ada na kuendelea kunitazama kwa utulivu akiwa anausubiri moshi uliojaa kinywani mwake upungue, ule unaokwenda kuyaharibu mapafu yake uende na ule unaotoka nje utoke.








Lilikuwa ni jambo la ghafula sana na lililonipotezea nguvu kwa muda mfupi.


"Likizo yako imesogezwa mbele....!"


"Kwanini mkuu?" Nilimuuliza kwa kihoro nikimtazama kwa makini usoni hata hivyo alikuwa kwenye utulivu wa hali ya juu sana akaipachika sigara yake kwenye midomo yake kama ada na kuendelea kunitazama kwa utulivu akiwa anausubiri moshi uliojaa kinywani mwake upungue, ule unaokwenda kuyaharibu mapafu yake uende na ule unaotoka nje utoke.


"Ni wiki sasa hii inakatika tangu kuanza kwa kikao kizito kilichofanyika Ikulu, muheshimiwa Rais hataki kuamini kabisa kama watu wake muhimu wamepoteza maisha hili jambo hataki kabisa kuliamini na kila alivyopewa ushahidi kuwa watu wale hawako hai alikataa na amegoma kusikiliza hizo hoja. Kikao hicho kilikuwa kizito sana na kilisimamisha shughuli zote muhimu za kimaendeleo za muheshimiwa Rais ikiwemo kumalizia ziara yake ya mwisho ya mkoani Manyara kwa ajili ya kuhakikisha majibu dhidi ya tuhuma za kupoteza maisha kwa watu hao wawili na muhimu kwa taifa yanapatikana kwa uzuri." Akatulia Daniel Matia Okale na kunitazama usoni huku moshi wa sigara ukitoka kinywani mwake. Alitaka yale aliyoyazungumza yaweze kuweka makazi katika akili yangu. Alinitazama kwa kitambo kama aliyekuwa akinitathmini na kuutathmini uelewa wangu kuhusiana na maneno yake kisha akaendelea.


"Daktari Lumoso Papi Mmbai na Daktari Omary Maboli Siki hawajapoteza maisha....!"


"Hata wewe unaamini kuwa hawajapoteza maisha mkuu?" Nikamuuliza mkubwa wangu wa kazi mwalimu Daniel Matia Okale huku nikimtazama kwa ukaribu sana. Alikuwa akivigongagonga vidole vyake vya mkono ambao haukuwa umekamata sigara pale mezani kwake kiasi cha sauti ya ka, ka, ka! Ikisikika ikitoka kwa awamu kwa kupishana kwa sekunde mbili ama tatu tafakuri nzito ikiwa kichwani mwake. Wakati akiwa anawaza mimi nilikuwa nikimtazama tu usoni huku mara chache nikiitazama ile sigara jinsi ilivyokuwa ikiteketea kwenye pacha ya vidoke vyake vya mkono wa kushoto bila kuijali. Nikamsikia akihema kwa nguvu kabla ya kuipachika ile sigara kwenye kingo za midomo yake akavuta kwa nguvu na kuutoa moshi kwa pembeni ya kinywa chake akanitazama.


"Hoja ya muheshimiwa Rais ilikuwa nzito sana na iliyoshiba, kila mmoja alivyoitafakari hoja hiyo akaamini akiwa na yakini kichwani mwake kuwa kweli Dr. Lumoso Papi Mmbai na mwenzake Dr. Omary Maboli Siki hawajafa." Akazungumza kwa utulivu mkubwa.


"Hoja hiyo iliegemea kwenye nini hasa hadi kupelekea mukubaliane nayo?" Nikamuuliza swali nikiwa makini zaidi ya awali.


"Kudorora kwa uchunguzi wa jambo hili katika awamu zote hizo na inavyoonekana kuna ujinga ulikuwa ukifanyika kwa kila ambaye anapewa kazi hii ya uchunguzi kuna jambo baya la kuzorotesha huwa linafanyika hili moja kwa moja limempa mawazo mapya mkuu wa nchi kuwa wataalamu wake aliyokuwa akiwategemea sana katika uchunguzi wa magonjwa au vimelea ibukizi vya magonjwa hatari ya kuhatarisha usalama na maisha ya wanadamu kwa ujumla, wapo na baadhi ya wanausalama wasiyowaaminifu wanajua hili lakini wanalifumbia macho pengine kwa kuahidiwa pesa nyingi ama wamelipwa tayari pesa hizo." Nilimtazama mwalimu Daniel Matia Okale mara baada ya kuongea maneno hayo. Mwili wangu niliuhisi ukichemka mithili ya mafuta ya ndafu ichomwayo kwa utaalamu mkubwa. Nilihisi jambo fulani la hatari sana lililolukuwa mbele yangu moyo wangu ukapata mashaka makubwa sana kupitia maneno hayo ya mwalimu Dao hata hivyo haikuwa hofu ya kushindwa kuyatafakari maneno hayo. Akili yangu ikafanya kazi ya haraka sana kuanzia jinsi madaktari wale walivyokuwa wakipata maneno ya vitisho hadi upotevu wao. Ilikuwa imepita miaka mingi tangu jambo hilo litokee hata hivyo kumbukumbu ilijirejesha kwa kasi ya ajabu sana kichwani mwangu.


"Nimeanza kukuelewa mkuu, nakumbuka kupitia taarifa moja ya kiuchunguzi iliyowahi kufanywa na baadhi ya wapelelezi waliyokuwa wameteuliwa kwenye uchunguzi huo, ikisema kuwa Dokta Lumoso Papi Mmbai alitekwa akiwa kwenye chumba chake cha uchunguzi wa kitabibu kilichopo nyumbani kwake nyuma ya soko dogo la Kikundi....!"


"Hiki ndicho pekee kilichonifanya leo hii nikupigie simu na nikuite hapa, kichwa chako ni chepesi sana na Hussein Babu hakuwa amefanya makosa kukufanya mbadala wa Rajab Omair Isihaq kuna mengi aliyaona kwako na ndilo pekee ninaloliona sasa." Akazungumza mwalimu Daniel Matia Okale akiwa na tabasamu pana huku akikitupia kipisi cha sigara kwenye kile kikombe akanitazama. Nikamuona jinsi kifua chake kipana na imara kwa kukijali kwa mazoezi ya kujali muda kikipanda na kushuka nikajua amepata utulivu wa nafsi baada ya kumuelewa.


"Maazimio ya kikao hicho ni yepi?" Nikamtupia swali huku nikijiweka kwenye kiti vizuri na kuegemeza mgongo wangu nyuma ya kile kiti nikamuona akinitazama katika hali ya kidadisi kidogo kisha akavuta mtoto wa meza na kutoa pakiti ya sigara ambayo ilionekana kuwa haikuwa imetumika sana. Nikamsikitikia sana mwalimu Dao kwa jinsi alivyokuwa akiyaharibu vibaya mapafu yake kwa moshi wa sigara huku akijitia hamnazo. Akatoa sigara moja na kuibana kwenye kingo za midomo yake akiitupia ile pakiti pembeni kisha kuchukua kiberiti cha gesi na kuilipua kabla ya kuvuta kwa nguvu na kupuliza moshi nje.


"Maazimio....!" akasema.


"....Maazimio yaliyofikiwa ni kwamba ile tume ya watu wane iliyokuwa imeundwa hapo mwanzo na wanausalama iendelee kufanya uchunguzi ama kwa namna nyingine ni kwamba ianze kufanya uchunguzi upya utakaoleta majibu mazuri kwa muheshimiwa Rais." Nilishtuka sana nilivyosikia jambo hilo hata hivyo mwalimu Dao akaendelea.


"Utaratibu ni ule ule kuwa wa mwanzo ambao kwa sasa hawapo kwa sababu za lazima za kimaradhi au kifo, nafasi zao huchukuliwa na mtu mwingine hata hivyo wapo ambao walikuwapo mwanzo na hata sasa wametumbukizwa kwenye uchunguzi huo."


Inawezekana vipi Paka apewe supu ya Samaki ailinde ilhali ana masiku kadhaa hajatia kitu kinywani? Niliwaza. Lilikuwa ni jambo la kushangazangaza sana lakini mwalimu Daniel Matia Okale akawa ameuona mshtuko wangu akanitazama huku akiubandua mgongo wake kitini baada ya kuuegemeza kwa muda na kuukita mkono wake mmoja mezani huku akiupuliza moshi wa sigara kwa madaha kama kwamba kufanya vile ni njia moja wapo ya kumuingiza kwenye ufalme wa Mungu.


"Hayo hayakuwa maamuzi ya kijinga hata kidogo." Akafungua kinywa chake.


"Unamaanisha nini?" Nikauliza huku sasa nikipata ari ya kufanya kazi maana dalili za kukabidhiwa kazi hiyo nilishaziona.


"Kikao cha pamoja kwisha na kufikia maamuzi hayo ya kuwaingiza wale wanausalama katika upelelezi wa kupeleleza tena upotevu wa madaktari waliyopotea katika mazingira tata, wakaaminishwa kabisa kuwa maazimio yalikuwa ni yale na hakukuwa na mjadala mwingine hata hivyo usiku wa jana kilikaliwa kikao kingine cha maamuzi ya kweli kutoka kwa watu wawili ambao muheshimiwa Rais anaimani nao na anaowategemea. Nilikuwapo mimi pamoja na mkuu wa ngazi ya juu kabisa ya usalama wa taifa kwenye masuala ya sheria bwana Athuman Maunge Kidaru akiwepo na muheshimiwa mwenyewe." Akaweka tuo mwalimu Daniel Matia Okale akavuta pafu moja la sigara yake kabla ya kukung'uta majivu kwenye kile kikombe kizito na kunitazama akaendelea.


"Athuman Maunge Kidaru ametoa wazo kuwa kazi hii ya kupeleleza maisha ya wataalamu wetu ikabidhiwe kwenye ofisi yangu, wazo hilo likajengewa hoja nzito ambayo ilileta majibu kuwa kazi hiyo niifanye mimi. Hapo hapo tukiwa tunajua kabisa kuwa kitengo cha usalama wa taifa kimetoa vijana kwa ajili ya kazi hiyohiyo chini ya mkuu mwenzake Mwambije Mkami. Umeona jinsi kazi hii ilivyo na mzunguuko usioleweka? Unahitajika umakini hapa. Kazi hii sasa iko mikoni mwetu Catherine na inaaza rasmi kuanzia sasa hivyo huna sababu ya kuifikiria likizo yako bali unachotakiwa kukifanya sasa ni kujua ni wapi unaweza kuanzia ili upate mwanga wa kazi yako. Safari hii wewe ndiye utakayekwenda kwenye kulichimbua hili baada ya kuwa Roi hayupo nchini." Akaniambia mkuu wangu nikatafakari kwa muda kidogo kabla ya kumuuliza.


"Kwanini iwe ni Ungamo moja kwa moja na isiwe sehemu nyingine?" Nilikuwa mtulivu sana, Daniel Matia Okale alinitazama kwa muda kisha akasema.


"Ndiyo maana nikakuambia kuwa ufanye uchunguzi wako kwanza sijui utaamua kuanzia wapi kati ya kwa Dr. Lumoso Papi Mmbai au kwa Dr. Omary Maboli Siki hata hivyo ni lazima uhakikishe unapo pa kuanzia. Nimejaribu kupitia kwenye chunguzi zilizopita ndipo nikaweza hisia zangu kwenye wazo hilo ila ni vema ukatafuta kwanza kabla ya kupitisha maamuzi, kesho asubuhi tukutane hapa ili nikupe maelekezo ya mwisho ya nini cha kufanya." Akaniambia mwalimu Dao. Sikuwa na swali jingine kwa wakati huo nikabaki nikiitazama Rafu ya vitabu huku nikiupitisha ukimya mfupi. Mwalimu Daniel Matia Okale alikuwa akiendele kuyaharibu mapafu yake bila huruma kwa sigara yake iliyokuwa ikielekea ukingoni akinitazama katika hali ya kunihurumia huku akiachia tabasamu jepesi la kunipa matumani ya kile nitakachokwenda kukifanya. Niliitazama saa yangu kwa wakati huo ikaniambia kuwa ilikuwa imeshatimia saa mbili usiku, muda huu ulikuwa ni mzuri sana kuanza uchunguzi wangu hivyo nilinyanyuka kutokea pale kitini na kumuaga mwalimu Dao kisha nikamuacha na kuufuata mlango huku nikiamini macho yake yalikuwa yakinitazama bila shaka lolote, nilipofika pale mlangoni niligeuka na kumtazama alikuwa bado akitabasamu nami nikatabasamu katika namna ya kumuondoa shaka. Niliufungua mlango na kujitoa nje ya ile ofisi na kuifuata lifti ambayo ilinirudisha jengo la chini kisha nikatoka baada ya mlango kufunguka nikiifuata ile korido ndefu.




_______




NILIRUDI PALE ROMBO WHITE BAR ambako niliegesha gari langu nililitazama eneo lile katika namna ya kulichunguza sasa nikaona jinsi palivyoanza kubadilika, gari ziliongezeka eneo lile sambamba na pikipiki, wingi wa watu waliokuwa wanafika hapo kupata burudani ulikuwa mkubwa sana. Nikalifikia gari langu na kuushika mlango nikiwa na lengo la kuufungua hata hivyo nikasita kwanza kisha nikageuza macho yangu kutazama pale kwenye mlango wa kuingia kwenye baa ile nikaona watu wawili wakiingia alikuwa ni kijana mmoja mrefu akiwa sambamba na binti mrembo aliyevaa sketi fupi iliyokomea chini kidogo ya magoti huku juu akiwa amevaa fulana nyeupe. Akili yangu ilifikiri vingi kwa wakati huo hata hivyo kitu pekee kilichonifanya niutazame ule mlango ni uhitaji wa jambo fulani ambalo huwenda kama ningelifanya kwa wakati ule ningejipotezea muda tu na nisingringiza chochote lakini moyo ukanisukuma niusogelee ule mlango wa ile baa hivyo sikuona haja ya kupoteza muda eneo lile hivyo nikaanza kuzitupa hatua zangu kuufuata ule mlango nikiliacha gari likizidi kunishangaa kwa namna nilivyobadili maamuzi. Niliingia bila kuwa na shaka yoyote macho yangu nikiyatembeza kila kona ya baa ile. Kulikuwa na watu wengi kiasi huku maongezi yasiyokuwa na utaratibu yakileta zogo dogo mule ndani. Kulikuwa na runinga kubwa kama ubao wa kuandikia ikiwa ukutani huku muziki wa bolingo ukiwa unaendelea kuchezwa, viti na meza vilivyopangwa katika utaratibu mzuri ambavyo vingi vilikaliwa na watu huku vichache vikiwa vitupu. Asilimia kubwa ya watu walikuwa wamekaa katika jozi ya wapenzi lakini iliyobakia iligawanyika kukiwa na vikundi kadhaa vya watu watano huku wengine wakiwa ni mtu mmoja mmoja. Nilijiingiza humo ndani huku macho ya baadhi ya watu yakinifanya ni sehemu yao nyingine ya burudani vijana hawakuacha kunitazama kwa jinsi ambavyo nilikuwa nikitembea na mavazi niliyokuwa nimevaa sikujali mtazamo wao nilikisogelea kiti kimoja na kumuita muhudumu huku bado nikizidi kutalii mule ndani taratibu. Niliagiza kinywaji na kutulia kilipoletwa nilikinywa taratibu bila purukushani kichwani mwangu jazanda kubwa ya kazi iliyopo mbele yangu ikaanza kujengeka. Nilifikiria vingi juu ya kazi ambayo sasa kwa asilimia kubwa hakuwepo mtu mwingine wa kuifanya zaidi yangu. Niliwafikiria madaktari hao wawili ambao kwa mtazamo wa ziada ilihitaji akili nyingi kuliko nguvu ili kujua nini kingeweza kuwa ni cha kuanzia kabla ya jingine kufuati. Ni miaka mingi ilipita na suala hili ni kama lilifunikwa na wanaojua kuitenda kazi yao hata hivyo hili la muheshimiwa Rais kuhitaji uchunguzi ufanyike upya lilikuwa ni suala la kustaajabisha sana.


Kwanini atoe...atoe amuzi hili mkuu wa nchi? Nilijiuliza pasipo kuwa na uhakika wa majibu.


Nilikuwa nimeikata chupa ile ya pombe vya kutosha sana na bado niliona kuna umuhimu wa kuagiza nyingine ili kuweza kuikata kiu yangu vilivyo hata hivyo sikuwa na muda. Tayari ilikuwa ni saa tatu juu ya alama usiku. Nikaushusha mkono uliyobeba saa yangu baada ya kutoka kuyatazama majira kisha nikainyanyua chupa na kukimimina kimiminika chote kinywani mwangu na kukimeza kwa utaratibu huku wazo la nini kilichopo mbele yangu kikiumbika tena kichwani mwangu. Muhudumu alikuwa kama anayeyasoma mawazo yangu kwani alifika pale na kuniuliza kama ningehitaji kuongeza kinywaji kingine nilitabasamu nikimtazama, alikuwa ni binti mrembo aliye katika sare zake za kazi ya sketi fupi iliyoishia juu kidogo ya magoti ya rangi nyeusi iliyoweza kuyaonesha mapaja yake mazuri manene kwa uchache na shati jeupe la mikono mirefu.








Muhudumu alikuwa kama anayeyasoma mawazo yangu kwani alifika pale na kuniuliza kama ningehitaji kuongeza kinywaji kingine nilitabasamu nikimtazama, alikuwa ni binti mrembo aliye katika sare zake za kazi ya sketi fupi iliyoishia juu kidogo ya magoti ya rangi nyeusi iliyoweza kuyaonesha mapaja yake mazuri manene kwa uchache na shati jeupe la mikono mirefu. Sikumjibu kitu badala yake nikatoa pochi yangu nikaifungua na kutoa noti ya shilingi Elfu tano akaipokea huku akisikiliza kama ningehitaji kinywaji kingine nikatazama saa yangu akaelewa nini maana yangu akaondoka na muda mfupi baadaye akarudi na kunikabidhi kiasi changu cha pesa kilichosalia. Nilinyanyuka baada ya kuuchangamsha mwili kwa kiasi fulani na kuelekea maegeshoni. Sikutaka kuifuata barabara niliyo jia hivyo nikawa nafikiria njia ambayo ningeweza kupita ambayo ingenifikisha Kikundi sokoni. Baada ya tafakuri fupi kupita kichwani mwangu nikawa nimeweza kupata wazo na maamuzi sahihi niliwasha gari langu na kuliondoa taratibu hapo nikiliingiza barabarani nikiiacha baa hiyo ya Rombo white nilipofika mbele kidogo nikakunja kulia kisha kushoto nikazidi kuifuata barabara hiyo huku nikikunja tena kulia nikiwa nimeliacha mbali sana Duka la Dawa la Amani, sasa nikawa nimeikuta barabara ya Sua. Nikachukua uelekeo wa upande wa kulia nikirudi mjini kabla sijafika kwenye mzunguuko wa barabara hiyo ya Sua nikawa nimefika kwenye Soko la Kikundi soko ambalo hufanywa biashara nyingi mchanganyiko na biashara zake huwa zinafanyika hata nyakati za usiku wakati mwingine. Nilitafuta mahali pa kuweza kuegesha gari langu. Niliyazunguusha macho yangu kwa udadisi sana nikaliona eneo moja tulivu nikaegesha gari langu hapo kabla sijateremka kutokea garini, nikalitathimini kwanza eneo hilo. Watu walikuwa ni wengi wakipishana wengie wakienda hivi na wengine wakienda vile niliporidhika na tathmini yangu nikaegesha gari langu kisha nilijitoa garini na kuufunga vizuri mlango wa gari yangu Toyota Corolla kisha nikaanza kujichanganya na watu wa eneo hilo. Ilionekana watu walikuwa wakianza kuondoka mmojammoja kutokana na muda kusonga sana na hali ya hewa kuwa tishio kwa majira hayo, wingu zito lilikuwa limetanda angani na tayari hali ya umanyumanyu ilokuwa imeshaanza. Sasa ilikuwa ikikimbilia saa nne usiku kwa mujibu wa saa yangu ya mkononi. Bidhaa nyingi zilikuwa zikiuzwa mahala hapo kama sumu ya Panya, mitego ya Panya, sabuni za asili zilizotengenezwa kwa miti shamba, nguo za mitumba, nguo za special, viatu vya mitumba, vya special, redio, kurunzi, urembo. Pia kulikuwako na matunda mbalimbali kama machungwa, matikiti maji, matango na kadhalika. Nilipita eneo hilo kwa hatua zangu za harakaharaka hata hivyo nilijionea vitu vingi. Nililiacha eneo hilo na kulizunguuka jengo moja la shirika la nyumba la taifa ambalo lilikuwa limepangishwa kwa watu wa kawaida. Upande huu wa pili haukuwa na pilikapika kabisa hivyo hali ya utulivu iliniridhisha nikazidi kuzitupa hatua zangu kulisogelea jengo moja ambalo lilikuwa kimya sana. Taa za nyumba hii zilikuwa haziwaki lakini kulikuwa na mwanga ambao ulikuwa ukitokea kwenye nyumba za jirani hivyo kulifanya eneo lote la nyumba hiyo kuonekana kwa urahisi. Kabla sijaifikia nyumba hiyo kwanza nilitazama usalama wa eneo hilo ili kuweza kujua kama kulikuwa na mtu yeyote aliyekuwa akizifuata nyendo zangu. Utulivu ulinitanabaishia kuwa ni mimi na pumzi zangu tu ndiyo tulikuwa eneo hilo.




Usalama ulikuwepo.


Nikatembea hadi kwenye baraza ya nyumba hiyo nikatazamana na mlango wenye kufuli kubwa, kabla sijausogele mlango huo kwanza niliupeleka mkono wangu mafichoni ili kuhakikisha kama silaha yangu ilikuwapo salama nilipojihakikishia kuwa ipo nikatoa glovu zangu na kuzivaa na kulishika lile kufuli kwa namna ya kulichunguza hata hivyo sikuambua chochote zaidi ya kujithibitishia uimara wa kufuli hilo. Nikatoa fungua zangu malaya na kuingiza moja baada ya nyingine kwenye tundu la ile kufuli muda mfupi kufuli lile likakubali sheria. Kumbukumbu ya kupotea kwa madaktari wetu wawili muhimu nchini ikajiunda tena kichwani mwangu mwili ukanisisimka sana huku nywele nikihisi zikipitiwa na kama upepo kwa jinsi zilivyokuwa zikisimama sikujiaminishia usalama wa kutosha hivyo nikapeleka mkono wangu chini ilipoishia Sketi yangu ya suti na kuupitisha mkono wangu hadi kwenye paja la mguu wa kushoto ambako nilichomoa bastola yangu kwenye mkanda maalumu wa kuhifadhia bastola nilioufunga pajani. Sasa nilikuwa nimeirudisha mkono baada ya kuwa niliirudisha mafichoni kwa ajili ya kukabiliana na lile kufuli kubwa. Niliitazama bastola hiyo niipendayo iliyotengenezwa huko U.S.A mnamo mwaka 1985 ambayo ilikuwa ikienda kwa jina la Browning Buck Mark. Silaha pekee miongoni mwa silaha kadhaa za aina hiyo ninazozikubali sana. Sikuwa na shaka nayo kwani magazini yake ilijaa risasi za kutosha. Nilivuta kitasa katika utaribu wenye kuleta utulivu na kutokuwaamsha majirani hatimaye nikausukuma mlango huo. Wazo la kuwasha taa lilinijia lakini sikulipa nafasi kutokana na kuleta maswali mengi kwa wapita njia watakaoiona hali hiyo ya kuwaka kwa taa na ilhali ni kwa takribani miaka karibia ishirini sasa nyumba hiyo haikuwahi kuwashwa taa na nyumba hiyo ilizuiliwa kutumika kabisa kwa kigezo kuwa bado uchunguzi wa kina ulikuwa ukifanyika hivyo wazo hilo nikalipiga teke na kupekuwa kwenye mkoba wangu ambako nilitoka na kurunzi yangu ndogo ya kijasusi yenye mwanga mkali sana na mwembamba ambao ungeweza kunisaidia kwa kiasi kikubwa kuihitimisha kazi yangu. Niliurudisha mlango nyuma yangu na kuufunga kabisa ili nisiwe na wasiwasi wowote nikiwa ndani.




Nyumba hii ilikuwa imepangiliwa kwa mtindo wa kizamani sana hata samani zake bado zilikuwa za kizamani. Kulikuwa na makochi matatu sebuleni hapo ambayo yalikuwa na foronya zenye rangi nyekundu huku zikiwa bado zimetandikwa vitambaa vyake vya kufuma kwa mkono, hii ilimaanisha kuwa eneo hili halikuguswa kabisa kwa muda mrefu tangu kutekwa kwa Daktari Lumoso Papi Mmbai bingwa wa uchunguzi wa magonjwa mbalimbali na ugunduzi wa madawa hususan kwa magonjwa sumbufu. Ilikuwa ni hazina kubwa sana hii ndani ya nchi hii yenye uhitaji mkubwa wa wataalu tiba kama hawa ambao wamechukuliwa kizandiki pasipo kujali ni madhara gani yatabakia nyuma.


Haikubaliki asilani.




Mbele yangu kwenye kona moja kabla ya kuuvuka uwazi mpana ambao ulikuwa ukielekea jikoni kulikuwa na friji la kizamani fupi na pana la rangi ya maziwa ambalo lilionekana bado kudai upande wa kulia kulikuwa na rafu ndogo ya vitabu vya kitabibu, vya riwaya mbalimbali na mafaili ya tafiti ya magonjwa mbalimbali na ya ripoti ambazo zilidhirisha kutimilika kwa uchunguzi wake, nikaisogele ile rafu na kuchukua kitabu kimoja nikakitazama kwa ukaribu nikagundua kuwa kilikuwa ni kitabu cha kibaoloji kilikuwa na vumbi sana kutokana na ukale wake wa kutokufanyiwa usafi, nikakiacha na kuchukua kingine hiki kilikuwa cha riwaya ya kipepelezi. Nikavuta picha ya mtu aliyekuwa akiishi ndani ya nyumba hii nikapata kujua jinsi ambavyo alikuwa hana muda uliokuwa ukipotea bure inawezekana muda mwingi aliumaliza kwenye tafiti zake vitabuni na kupata burudani muda mwingine na mchache uliobakia akiugawanya kwa vile ilivyokuwa inafaa kwa upande wake. Nilizidi kumfikiria mtu huyo huku macho yaliyokuwa yakipata msaada wa kurunzi yangu yakitazama ukutani na kukutana na picha tatu. Picha ya kwanza ikiwa ya kuchora tena ikiwa ni michoro ya kizamani ya kubuni iliyovutia kuitazama ambayo ilimuonesha mnyama mkubwa aliyekuwa amechorwa kwa ujuzi wa hali ya juu sana, picha ya pili ilikuwa ni ya kwake ya weusi na weupe ikimuonesha akiwa kwenye joho la rangi nyeusi lenye nakshi nyekundu kwa uchache sambamba na kofia kichwani hii ikanipa jibu kuwa huwenda ilikuwa ni kumbukumbu yake kubwa ya siku ya kuhitimu moja ya elimu zake za juu za kitabibu, picha ya tatu pia ilikuwa ni yake akiwa kwenye vazi la kitabibu huku akiwa amening'iniza kifaa cha kupimia mienendo ya mapigo ya moyo ya binadamu (Telescop). Alikuwa kwenye tabasamu pana sana. Bado mlolongo wa ujengaji wa picha wa Daktari huyu ulikuwa ukijengeka kichwani mwangu, alikuwa ni mtu mcheshi kwa muonekano wa picha zake zote mbili. Sasa nikayatoa macho yangu kwenye zile picha na kuendelea na ukaguzi wangu nikaona kulikuwa na meza pana sana hapo sebuleni na hii ikanivuta zaidi, ilikuwa ni meza ya kizamani ya umbo la mstatili fupi na nyembamba kwa mandhari ya hapa sebuleni tu ikatosha kujua kuwa Daktari Lumoso Papi Mmbai alikuwa bachela. Kila kitu kilipangwa kiumeume sana, nikaichunguza meza hiyo kwa kitambo kifupi kisha nikaachana na hapo sebuleni nikachukua uelekeo wa jikoni huko nikakutana na mtindo wa kipekee sana kwani hakukuwa na kabati la vyombo wala kifaa chochote ambacho kingeweza kuhifadhia vyombo. Niliona sufuria mbili safi na ngumu za kizamani kabisa ambazo zilikuwa zimetundikwa juu ya ubao mgumu ambao ulikuwa kama benchi fulani jembamba sufuria hizo ndani yake kukiwa na vikombe viwili na pembeni yake kukiwa na kibeseni kidogo ambacho kilibeba sahani mbili za udongo sambamba na bakuli moja. Picha hii inaweza ikamchanga mtu yeyote yule na kutokuamini kama muhusika wa nyumba hii alikuwa ni Daktari mkubwa na muhimu sana nchini hata hivyo kwa uzoefu wangu wa kazi hizi na kuchunguza maisha ya watu wengi na tabia zao, haikunisumbua kugundua kuwa Dokta Lumoso alikuwa ni mtu asiyependa kula nyumbani kwake mara kwa mara. Nikatoka humo ndani na kuingia kwenye chumba kingine hiki kikanifanya nigande kwa sekunde saba nzima mlangoni. Kilikuwa ni chumba cha kiuchunguzi hiki kilisheheni vifaa vingi vya kidaktari. Mbele yangu kwenye ukuta kulikuwa na rafu kubwa ya vitabu na mafaili mbalimbali hii bila shaka ilikuwa imesheheni mafaili mengi ya kiuchunguzi. Chumba hiki kikanivutia zaidi. Ukutani kwenye kuta mbili za kushoto na kulia kulikuwa na picha nyingi mbalimbali za ajabu ajabu zikieonesha mifumo mbalimbali kwenye mwili wa binadamu. Kulikuwa na picha iliyoonesha mfumo wa upumuaji, Moyo, mfumo wa umeng'enyaji chakula, mfumo wa uzazi wa kike na kiume, mfumo wa usafirishaji damu kupitia sehemu mbalimbali za mwili lakini pia kulikuwa na picha ya mifupa mbalimbali ya mwanadamu sambamba na picha ya Skeletones pamoja na picha ya mfumo mzima wa ubongo. Upande mwingine wa ukuta kulikuwa na picha za vifaa mbalimbali vya kufanyia uchunguzi wa kivitendo kama 'test tube' na kadhalika. Katikati ya chumba hiki kulikuwa na meza kubwa maalumu ya umbo la mstatili iliyotengenezwa kitaamu sana na hii ilikuwa ni maalumu kwa ajili ya uchunguzi wa kivitendo (Practical Experiments). Ubavuni mwa meza hiyo kulikuwa na kiti kirefu kilichokuwa sawia na meza hiyo, macho yangu nilizidi kuyatembeza mule ndani na niliporidhika na kuona kwangu nikaisogelea ile meza na kuikaribia kabisa. Juu ya meza hii kulikuwa na Tube mbalimbali zilizobeba Kemikali zenye rangi tofauto tofauti kama Buluu, kijani, njano, nyekundu, pinki, rangi ya Zambarau na nyinginezo, nyingi zilizoonekana kuwa zilikuwa kwenye mchakato wa kufanyiwa kazi kabla ya muhusika kutekwa. Picha hii ya mtazamo ikanisisimua mwili na kujiuliza kichwani mwangu kuwa kunauwezekano mkubwa nyumba hii isiwe imekaguliwa tangu kutekwa kwa mwenyeji wake? Hata hivyo nikakumbuka kuwa kulikuwa na chunguzi mbalimbali za kipelelezi zilifanyika. Hii ilikuwa na maana kuwa nyumba hii ilikaguliwa na kama ilikaguliwa basi; mkaguaji wake hakuwa mtu wa kawaida. Sikujali kuhusu hilo, bado nilikuwa na uhakika wa kupata kitu.




Kulikuwa na 'Silinder' mbalimbali, telescop, lens tofautitofauti kwa ajili ya kukuzia vimelea vya maradhi visivyoonekana kwa macho, jiko la kutumia mafuta, taa ya Karabai kubwa yenye mwanga mkali sambamba na vingine vingi.




Hii kweli ilikuwa maabara ya Daktari. Niliwaza huku nikimulika hapa na pale nikikung'uta vumbi kifaa hiki na kile katika namna ya kuchunguza huku nikizuia uwepo wangu kutokuonekana kama kungekuwa na mtu mwingine nyuma yangu. Nikaitazama saa yangu ya mkononi nikagundua kuwa muda ulikuwa ukiniacha sana, nikaliwazia gari langu mahali nilipoliegesha mawazo yangu yote ni kuhusiana na usalama wa mimi mwenyewe mahali hapo kama kungetokea mtu wa kutaka kujua ni kwanini gari hilo lilikuwa mahala hapo muda huo wa saa saba kwenda saa nane usiku. Mvua nayo ilishaanza kuleta shida huko nje kwani kelele zake zilikuwa zikiyasumbua masikio yangu matone yake mazito yalipokuwa yakitua kwenye bati hata hivyo nilifanikiwa kuukumbatia utulivu zaidi usiniponyoke ukenda zake. Nilikata tamaa kabisa baada ya kugundua kuwa nisingepata chochote cha kunisaidia labda. Sikuwa mjinga wa kuchukua maamuzi ya haraka ya kujiondokea mahali bila kupata chochote kwanza nilijipa imani kuwa hakuna mtu ambaye angeweza kulitilia mashaka gari langu kwani nililiegesha mahala ambapo yeyote ambaye angeliona angejua ni moja ya magari ya wakazi wa eneo hilo la watu wanaokaa ghorofani kwenye jengo lile la shirika la nyumba la taifa. Nikaanza kuitembeza kurunzi yangu kila mahali na kila kona hadi nyuma ya ile meza. Nikatabasamu kidogo baada ya kuona kitu kilichonifurahisha chini upande wa nyuma wa ile meza kulikuwa na uzi mwembamba sana ambao kama hauko makini huwezi kuuona ulikuwa mfano wa utando wa Buibui wenye rangi nyeusi ya kufifia kiasi kwamba uliendana na sakafu ya eneo hilo ambalo halikuwa limefunikwa kwa kapeti yoyote. Nikaufuatilia ule uzi nikagundua ulikuwa umepita pembeni kidogo ya mtoto wa meza ile kwa upande ule, nikainama chini huku nikiwa makini nisiitingishe ile meza wala kuweka alama yoyote mule ndani nikamulika kwa chini ya ile meza nikauona ule uzi umeishilizia kwenye kidude kidogo sana mfano wa mbegu ya Boga kikiwa na rangi nyeusi, tabasamu likawamba usoni mwangu. Nikaking'oa na kukiweka juu ya meza kisha nikaufuatilia ule uzi ambao ulipita chini kwenye ukuta hadi nyuma ya rafu ya vitabu nilipomulika kurunzi yangu nikaona redio kaseti ndogo ya kizani ya kurekodi ikiwa imejaa vumbi vibaya sana nikaichukua na kuifuta vumbi kisha nikaiweka juu ya meza huku nikivitazama kwa ukaribu vitu vile.






Tabasamu likawamba usoni mwangu. Nikaking'oa na kukiweka juu ya meza kisha nikaufuatilia ule uzi ambao ulipita chini kwenye ukuta hadi nyuma ya rafu ya vitabu nilipomulika kurunzi yangu nikaona redio kaseti ndogo ya kizani ya kurekodi ikiwa imejaa vumbi vibaya sana nikaichukua na kuifuta vumbi kisha nikaiweka juu ya meza huku nikivitazama kwa ukaribu vitu vile. Nikiwa naendelea kuitazama ile redio na kile kidude cheusi mfano wa mbegu ya Boga, mwanga mkali sana ukapiga kisha baada ya hapo lile wingu zito likawa limefika mwisho wa uvumilivu na kuyaona yale maji ya mvua yaliyokuwa yakimwagika na kunipa kero masikioni mwangu yalikuwa hayatoshelezi, kwani iliongezeka mvua kubwa ya kishindo sana. Nikaanza kujenga mawazo mapya ya matumaini nikiamini hii ingesaidia kunificha kwa namna moja ama nyingine.




Mungu ni mwingi wa miujiza yaani wingu hilo lilianza kutanda angani majira ya saa kumi saa kumi na moja na likadumu hadi muda huo, nilipoitazama saa yangu ilikuwa yapata saa sita na dakika kumi muda ulikuwa ukizidi kukimbia kwa kasi kubwa sana kwa kweli. Nikaachana na mawazo kuhusu mvua nikahamisha macho yangu tena pale mezani kisha nikafungua mtoto wa meza nikachangua hiki na kile katika namna ya kuona kama ningeweza kupata ziada lakini hakukuwa na kitu kingine cha maana. Nikaichukua ile redio na kwenda nayo sebuleni wazo la kuwasha taa ili niweze kuichunguza vizuri likanijia tena hata hivyo hali ya kiusalama ikanionya kwa mara nyingine tena. Nikazidi kuikung'uta vumbi na kuichunguza kwa karibu nikagundua kuwa ilikuwa ni redio iliyokuwa ikitumia kuchaji kwa umeme lakini pia inawezekana kuitumia muda wowote kama ukiichomeka kwenye umeme na kile kidude cheusi mfano wa mbegu ya Boga kilikuwa ni kinasa sauti makini sana hapo nikapata picha kuwa huu ulikuwa ni mpango kabambe nikajiuliza; Nani muhusika wa jambo hili? Ni Dokta Lumoso Papi Mmbai au wanausalama? Kama ni Dokta Lumoso, kwanini? Na kama ni wanausalama pia ndiyo walifanya hivyo nayo kwanini? Nikaweka tuo la mawazo yangu kisha nikatazama namna ilivyounganishwa kwa utaalamu wa kuungaunga.


Inamaana wanausalama waliwahi kuja kwenye nyumba hii kufanya upekuzi hawakuliona hili au...? Au ni wanausalama hao ndiyo waliyoweka hiki ili kugundua ujaji wa mtu mwingine humu...? Haya maswali mawili yalijengeka mara zaidi ya nyingi kichwani mwangu na nikatakiwa kujipa muda wa ziada kujijibu. Wazo kuhusu wanausalama kupanda hiki kinasa sauti likayeyuka kichwani mwangu hii ilikuwa na maana kuwa hata akili yangu iligoma kuamini.


Atakuwa ni Dokta Lumoso Papi Mmbai ndiye....ndiye amepanda hiki. Nikawaza.


Kama alikuwa ni Dokta Lumoso Papi Mmbai kwanini alifanya hivi....? Inamaana pengine alijua ujaji wa watekaji nyumbani kwake....? Kwanini alijua hili....? Kuna dalili gani zilikuwa zikimtanabaishia hilo....? Nikazidi kujiuliza hata hivyo maswali hayo yalikuwa ni kitendawili kikubwa sana kwangu.


Nisingeweza kujijibu nikiwa nabung'aza macho hapo mezani kamwe.


"Hapa kuna kitu kimefichikana na kinahitaji uchunguzi wa kina sana." nikajisemea mwenyewe huku nikifungua moja ya sehemu ya kuwekea mkanda, nikakuta mkanda na nilipouchunguza niligundua ulikuwa ikifanya kazi sawia. Haraka sana nikapata wazo la kwenda kuusikiliza kujua kuna nini ambacho kilirekodiwa na redio hiyo. Mvua ilikuwa imechachamaa sana huko nje hata hivyo haikuwa kikwazao kwangu kufikiri ningefanya nini kuweza kuisikiliza. Waya kilikuwa kikwazo, nikafikiri kwa haraka ningepata wapi waya ambao ungeweza kusaidia kuunganisha kwenye umeme ili niweze kusikiliza rekodi hiyo. Nilisha chakua kote na sikuona kitu cha namna hiyo nilipokaa kwa sekunde kadhaa nikitafakari akili yangu ikanituma nitazame juu ya ile rafu ndogo ya vitabu sebuleni, lile boksi dogo lililofungwa nikaliona likiwa palepale nikajua hilo sikuwa nimepata muda wa kulichunguza. Nikaisogelea ile rafu ya vitabu na kulishusha lile boksi halikuwa zito nikashangaa lakini pia nilikata tamaa ya kuweza kusikiliza rekodi hiyo kwa wakati. Nilipolitua mezani lile boksi nikalifungua ndani nikalikuta haliko kwenye mpangilio mzuri kwani lilichanguliwa sana lakini chini kabisa ya boksi hilo nikakutana na kitu nilichokuwa nikikihitaji. Tabadamu likauvamia uso wangu nikauchukua ule waya na kuelekea kwenye ukuta kwa kusaidiwa na kurunzi yangu nikaweza kuona sehemu ambayo ningeweza kuchomeka ule waya. Nikachomeka na kuiwasha ile redio bahati ilikuwa upande wangu iliwaka nikabofya kitufe cha kuurudisha mkanda nyuma hadi mwanzo kabisa kisha nikabofya tena kitufe cha kuuruhusu mkanda ucheze. Nilianza kusikia upepo na mgongano wa vitu kama chupa nikajua kuwa Dokta Lumoso Papi Mmbai alikuwa akiiruhusu hiyo redio irekodi hasa awapo kwenye chumba chake cha uchunguzi au awapo nyumbani kwake. Nilijipa uvumilivu sikutaka kukata tamaa hata kidogo, wakati nikiwa nasikiliza nikasikia sauti ya kikohozi ambayo mara kwa mara nilikuwa nikiisikia lakini hii utofauti wake ni kwamba ilikuwa ni katika maandalizi ya kumruhusu mtu huyo kuongea jambo.


"Kwenye rafu ya vitabu mstari wa pili chini kwenye uvungu wa rafu hiyo ya vitabu." Sauti ya mtu ilisikika redioni namna hiyo, nikayahifadhi hayo maneno hata hivyo ukimya ulirudi tena zile sauti za upepo na mgongano wa vitu kama chupa ukijirudia. Niliendelea kusubiri huku nikijipa utulivu mkubwa huku wazo jipya likijiunda kichwani mwangu dhidi ya hicho kilichowekwa chini ya uvungu wa rafu ya vitabu mule kwenye chumba cha uchunguzi pamoja na kuwaza sana lakini sikuwa nimepata cha ziada. Muda sasa ulikuwa ukizidi kukimbia kwa kasi kubwa sana zilishakatika dakika ishirini na kitu tayari. Nikarudishiwa umakini wangu baada ya kusikia sauti ya kishindo redioni, hii ikaniweka macho zaidi mara utulivu ukapita kwa jozi ya sekunde kadhaa kisha purukushani.


"Weka utulivu Dokta Lumoso Papi Mmbai, Dokta mahiri, Dokta bingwa wa masuala ya kiutafiti hah, hah, haaa!" Ilizungumza sauti ya mtu mmoja redioni hii ilikuwa bila shaka ni ya miongoni mwa watu waliokuja kumteka Dokta Lumoso.


"Nyinyi ni wakina nani na kwangu mnataka nini?" Sauti ya Dokta yenye hofu ikauliza huku ikilazimisha kuwa na utulivu.


"Wewe ukifikiria unadhani sisi tumekuja kufanya nini kwako....? Unadhani tumekuja kwa ajili ya kupata matibabu labda au kuja kupima magonjwa mbalimbali kama Gono, Kaswende, Pangusa, Ukoma au Kifua kikuu? Au unafikiria nini zaidi?" Niliendelea kuzisikia sauti za watu hao zenye majigambo makubwa na hadi hapo tayari nilishapata idadi ya watu waliyohusika na utekaji wa Dokta Lumoso Papi Mmbai walikuwa wawili mmoja akionekana kuwa mmbabe na mkorofi lakini huyu wa pili kusikika akionekana kuwa mvijivuni na mmbabe kwa mujibu wa maongezi yao kupitia rekodi hiyo.


"Ningekuwa najua nisinge wauliza na kinachonishangaza ni kwamba ujio wenu ni wa ghafula usiku wa saa sita namna hii hamuoni kwamba muda huu watu wamepumzika?" Niliisikia sauti ya Dokta Lumoso ikiwa katika utulivu sasa.


"Tunajua kuwa watu wamepumzika hata hivyo kwa mtu kama wewe anayefanya kazi kama Mchwa tuliamini utatupokea ungali macho." ile sauti ya mtu wa kwanza ikasikika tena.


"Mnashida gani na mimi usiku wote huu?" Dokta Lumoso Papi Mmbai akauliza.


"Musa anakuhitaji kwa udi na uvumba na ndiye aliyetutuma tukupeleke kwake!" Ikajibu ile sauti ya mtu wa pili ikiwa kwenye utulivu wa hali ya juu sana.


"Musa...? Huyo musa ni nani na kwanini amitume kwangu hajawapa sababu?" Akauliza Dokta Lumoso Papi akiwa kwenye utulivu mkubwa.


"Hiyo siyo kazi yetu kujua hivyo kwanini na kwanini alitutuma, kazi yetu sisi ni hii tunayokwenda kuitekeleza sasa....Mdaba fanya kazi yako!" Iliongea ile sauti ya mtu wa pili ikiwa kwenye ujivuni uleule kisha mwishoni ikatoka amri kuwa kazi ifanyike kilichosikika ni kelele hafifu za Dokta Lumoso Papi Mmbai zikiashiria maumivu kidogo aliyoyapata kwa purukushani hizo kisha kimya kikachukua nafasi yake baada ya hapo zikafuatia purukushani nyingine kama za mtitikano kisha sauti ya mlango kufungwa ikasikika.


"Musa! Ni nani huyu Musa...? na kwanini awatume watu wamteke Dokta Lusumo?" Nilijiuliza nikiwa nimekaa kwenye kiti ambacho nilikisogeza hapo ukutani ili kuweza kujipa utulivu katika kusikiliza pasipo kujali vumbi lililotapakaa kwenye kiti kile. Nikayatafakari maswali ya Dokta Lusumo nikajua yalikuwa na maana kubwa sana na pia nikajihakikishia kuwa yeye ndiye aliyepanda hiki kifaa kilichoundwa katika ujuzi wa hali ya juu sana ingawa haukuwa katika ubora wa kifunfi ila ulileta muonekana wa juhudi zake ili kuweza kuchukua sauti kwa uhakika hata kama muongeaji angekuwa ananong'ona. Kumbukumbu za maelekezo ya Dokta Lusumo yakajijenga kichwani mwangu haraka sana nikaichukua ile redio na kile kifaa cha kunasia sauti kisha nikafungua mkoba wangu na kutoa mfuko mweusi wa nailoni na kutumbukiza ile redio na kile kifaa kisha nikaviweka ndani ya mkoba wangu na kurudisha kiti mahali pake huku nikihakikisha kila kitu kinakuwa katika usiri. Nilielekea kwenye kile chumba cha uchunguzi wa kitabibu na kuanza kuyatembeza macho yangu kwa umakini mkubwa huku yakiwa yanasaidiwa na mwanga mkali wa kurunzi yangu ya kijasusi (penlight). Mvua haikuacha kunyesha huko nje na ilizidisha kasi yake katika unyeshaji. Nikaitazama saa yangu nikajua nilitakiwa kufanya haraka zaidi kwani bado nilikuwa na kazi ya kuhitimisha usiku huo huo, nilisogea hadi pale ilipo ile rafu ya vitabu na kusogeza huku na kule vikorokoro na mabundu yaliyofungwa fungwa kisha nikatumia nguvu zangu kuisogeza ile rafu ya vitabu vya kitabibu na uchunguzi wa kitalamu pembeni huku nikiwa nimeweka chini bastola yangu matata Browning Buck Mark sambamba na kurunzi. Niliviokota kisha nikairudisha bastola yangu kwenye maficho yake huku nikitumia kurunzi kuchunguza kilichopo pale chini. Niliona faili moja likiwa limekaa pale chini likiwa halijulikani ni la rangi gani kutokana na kuzongwa na vumbi pamoja na utando wa Buibui nikaliokota kwa uangalifu mkubwa kisha nikalifuta uchafu wote na kulichunguza vizuri. 'MPANGO WA NJE' Lilikuwa limeandikwa hivyo faili hilo juu kwenye kava lake ngumu.


Nini hii? Nikajiuliza pasipo kujua namna ya kupata majibu. Akili yangu ikarudisha kumbukumbu nyuma na kuyakumbuka maneno ya mkuu wangu wa kitengo cha kijasusi mwalimu Daniel Matia Okale. Ile kauli kuwa kuna uwezekano wa kwenda mimi nchini Ungamu ikajiunda kichwani kwa namna ya kunikumbusha. Nikahusianisha na maneno ya juu ya hilo faili, nikaafiki kuwa huwenda kweli huu ulikuwa ni mpango wa nje.


Kivipi...? Nikawaza tena hata hivyo sikutaka kujichosha, nikalifunua ndani na kukuta hati za mikono huku chache zikiwa zimechapwa, iliandikwa kwa maandishi ya kitabibu zaidi hata hati yake ilikuwa ni ya kitabibu na zile zilizochapwa angalau niliweza kuelewa lakini si katika ufafanuzi. Sikutaka kupoteza wakati nilirudisha kila kitu kama nilivyokikuta kisha nikatoka hadi sebuleni nikiwa na lile faili mkononi ambako nako niliweka vitu katika usawa nilipojiridhisha na hali ya mule ndani kuwa hakuna mtu atakayegundua ujaji wangu nikatoka nikiizima Kurunzi yangu na kuitia kwenye mkoba. Nilipotoka nje, nilipokewa na mvua kubwa sana iliyokuwa ikinyesha kwa sifa kubwa hata hivyo sikuwa na namna na sikuona sababu ya kukaa hapo tena. Nilishaufunga mlango hivyo niliambaa na baraza ya nyumba hiyo hadi ukingoni mwa baraza hiyo ambako nilitumia koti langu la suti kujifunika kichwani ili kuzuia maji ya mvua yasiweze kuathiri nywele zangu, nikakimbilia kwenye nyumba nyingine ya jirani ili kuweza kujizua kiasi nikaambaa na baraza pia hadi nilipoweza kuliona gari langu likiwa katika hali ya upweke. Nikapiga mahesabu ya hatua kwa umbali wa kutoka hapo hadi lilipo jengo moja la ghorofa ambalo nilipanga kuambaa nalo hadi ilipo gari yangu. Nikazivuta hatua zangu kwa haraka na kulifikia jengo hilo kisha nikaambaa nalo hadi nilipolifikia nikalitazama kwa namna ya kulichunguza na nilipojiridhisha na usalama wake, nikaingia na kutulia kidogo nikiyachunguza mazingira ya hapo. Sikuwa na shaka na usalama wa vitu nilivyovibeba kwani mkoba wangu wa ngozi ulikuwa imara.




*_______*




Mtaa huo ulikuwa umetulia sana kiasi kwamba sikuweza kuona mtu wa aina yeyote kukatiza nikazidi kutuliza macho yangu vizuri ili kupata uhakika, kwenye baraza ya jingo moja kutoka kwenye lile jengo refu la ghorofa la shirika la nyumba la taifa kwa umbali wa kama hatua arobaini na tano za mtu mzima mwenye urefu wa futi sita, niliona kivuli cha mtu kikiwa kimejilaza barazani na kwa umbali niliopo kilionekana ni kama kifurushi fulani tu kilichotelekezwa. Sikutaka kujiridhisha kwa dhania kuwa mtu yule angekuwa amelala kweli. Nikajipa utulivu zaidi ili kupata kujiridhisha kwa uhakika, nilipotulia kwa muda wa kama dakika moja zaidi macho yangu yakaweza kulizoe giza hafifu la eneo hilo na kunionesha kuwa kile kifurushi kilikuwa ni mtu.






Sikutaka kujiridhisha kwa dhania kuwa mtu yule angekuwa amelala kweli. Nikajipa utulivu zaidi ili kupata kujiridhisha kwa uhakika, nilipotulia kwa muda wa kama dakika moja zaidi macho yangu yakaweza kulizoe giza hafifu la eneo hilo na kunionesha kuwa kile kifurushi kilikuwa ni mtu.




Ni hawa wenye maradhi yasababishwayo na utumivu wa kijinga wa dawa haramu za kulevya ambao hawana mahali maalumu pa kulala au? Nilijiuliza hata hivyo nikapata wazo la kumulika kwa kutumia taa za gari langu kwani gari langu taa zake zilikuwa zikielekea mtu yule alipo. Nikaliwasha na kuwasha taa 'full' kwa muda kidogo kabla ya kupunguza mwanga, ile ilitosha kunijulisha kuwa alikuwa ni kichaa au mwenda wazimu kwa lugha tamu ambaye alijihifadhi mahala hapo kuikwepa adha ya mvua kubwa iliyokuwa ikiendelea na kuupisha usiku huo ili kuchapo aendelee na taratibu zake za kimaisha. Sikupoteza muda tena niliondoa gari taratibu na kurudi nyuma kidogo na kuingia barabarani kisha kuufuata mzunguuko wa barabara ya Sua kisha nikaifuata barabara ya upande wa kushoto nikaongeza kasi ya gari nikiipita Top Life Bar and Resturant, hapakuwa na watu wengi sana eneo hili bali magari machache tu yaliyokuwa yameegeshwa, niliifuata hiyo barabara nikilipita jengo la Tex Palace kisha Masika Pharmacy kabla sijaipita ofisi kuu ya Tanesco mkoani hapo hadi shule ya msingi Msamvu. Bado mvua haikutaka kuacha kabisa na haikupunguza hata kasi ya unyeshaji wake, nikiwa naukaribia mzunguuko wa barabara ya Msamvu, fikra zangu zikarudi tena nyumbani kwa Dokta Lumoso Papi Mmbai niliwaza mengi baada ya kurudisha fikra zangu huko lakini kubwa ni kuhusiana na watekaji au waliohusika na upotevu wa madaktari hawa waaminifu wanaotegemewa na serikali. Nilifikiria sana kuhusiana na hilo bila kupata majibu stahiki kwa kweli ilikuwa ni lazima kuhakikisha hili linapatiwa ufumbuzi wa kina kuhusiana na upotevu wao, kama wamekufa basi ijulikane sababu kuu ya kuwaua ni nini na wapi yalipo makaburi yao. Nilizidi kuwaza huku nikiupita mzunguuko wa barabara ya Msamvu kisha kukipita kituo cha kujazia mafuta cha Oil Com kabla ya kituo kikuu cha mabasi Msavu nikiwa nimechukua uelekeo wa Kihonda nikakunja kulia huku jina la Musa likinijia tena kichwani.




Musa...! Musa ni nani hasa...? Inamaana hili limeshindwa kugundulika kweli kwa miaka yote iliyopita...? Miaka zaidi ya kumi na nane sasa...? Hapana. Nilijionya kwenye mawazo yangu kuwa sidhani kama kwa kipindi chote hicho wanausalama wengi waliyowekwa kwenye uchunguzi huu washindwe kuling'amua hilo na pia nilishindwa kujipa majibu ya uhakika kuwa ni kwanini wale waliyoshindwa kuleta majibu ya uchunguzi wao warudishwe tena kwenye uchunguzi huu tena ikiwa watu ambao mnyororo wake ulikuwa ni wa hawahawa waliyoshindwa.




Kwanini muheshimiwa Rais ameamua jambo hilo...? Pia nalo pamoja na kujiuliza sikupata mwangaza walau wa jibu. Nilisimamisha gari mbele ya Makuti Bar kisha kabla ya kuizima nikapoteza muda mdogo kuweza kuishangaa mandhari ya eneo hilo. Nilijua tu kwa muda huo ni vigumu sana kukuta watu hata hivyo haikuwa sababu ya mimi kujipa uhakika wa kushindwa kujipa imani kuwa eneo hilo ni salama. Nilizidi kulichunguza hadi nilipojihakikishia usalama ndipo niliposhuka na kuufunga mlango wa gari vizuri na kupiga hatua za haraka kuliacha eneo hilo. Nilifika mbali na baa hiyo na sasa nilikuwa nikitazamana na mlango wa nyumba moja ambayo nayo ilikuwa haitofautiani na ile ya Dokta Lumoso. Si kwa muundo wa ujenzi wake au mtindo wake wa kiezekeo la hasha! Ukimya na giza, hakukuwa na utofauti kwenye hilo. Nikaufungua mlango wake kwa mtindo uleule na kuingia ndani hii haikuwa kwenye utulivu kama ile niliyotoka. Kwa kutumia Kurunzi yangu niliweza kuona jinsi ustaarabu ulivyo vunjwa kwenye sebule hiyo. Foronya za kizamani zilikuwa zimetupwa chini huku makochi yake yakiwa uchi, utaratibu huu ukanishangaza zaidi na kunipa umakini wa hali ya juu sana tayari bastola yangu ilikuwa mkononi nimeishika madhubuti nilipenda zaidi kujihami kuliko kujiamini sehemu yenye mashaka. Kanuni zangu za mafunzo ya kijasusi yalinitaka niwe makini kila mahali. Sebule haikuwa ikitazamika kabisa, meza ilikuwa imewekwa sehemu ambayo haikuwa mahala pake, zulia dogo la malighafi ya mkonge iliyokuwa imetandikwa hapo sebuleni ilikuwa imefunuliwa na kukunjwa kabisa. Niliichunguza kwa makini sana sebule hiyo ambayo kwa muonekano haikuwa ikitofautiana na ile ya nyumba niliyotoka muda mfupi nyuma. Ukutani niliona picha moja kubwa iliyo ndani ya Fremu ikimuonesha Dokta Omary Maboli Siki akiwa kwenye suti safi ya kijivu iliyoshonwa kizamani huku kichwani akiwa ametupia kofia ya pama machoni akitundika miwani ya macho. Alikuwa katika muonekano mzuri sana na wa kuvutia nilipoyatupia macho yangu kwenye rafu ya vitabu, nikaona jinsi vitabu vilivyo changuliwa huku vingine vikiachwa chini sakafuni. Hali hiyo ikazidi kunitahadharisha zaidi. Nikaiacha sebule hiyo na kuelekea chumbani ambako kulikuwa na kitanda kimoja cha futi nne kwa sita ambacho kilifunuliwa godoro lake huku shuka zikiwa chali, panga boi ambalo lilijaa tandabui pamoja na vumbi huku likionekana kuanza kupatwa na kutu, Droo ya kitanda ilikuwa imefunguliwa na chini kukiwa na pakiti la sigara kali au sigara nyota almaarufu, likiwa limetelekezwa na bidhaa zake, uvungu wa kitanda hicho ulikuwa mchafu sana. Wakati nikiwa nachunguza zaidi, nikakumbuka nyumbani kwa Dokta Lumoso Papi Mmbai sikuwa nimefanya upekuzi chumbani na laiti kama nisingepata ule ujumbe wa maelekezo, ningekuwa nimefanya kosa kubwa ambalo ningelijutia na ingenibidi kurudi kivyovyote vile.


Sikuwa na shaka tena.




Sikupoteza muda wangu kuendelea kutazama huko uvunguni badala yake nikaendelea na sehemu nyingine ambazo nazo hazikunipa kitu kipya. Nikakiacha chumba hicho na kuhamia kwenye chumba kingine ambacho kilifanana na kile cha Dokta Lumoso utofauti wa hiki na kile ni kwamba hiki kilikuwa kimechanguliwa mbaya zaidi ni kwamba mafaili na vitabu vingi vikiwa vimetupwa sakafuni.


Nilichoka kabisa.




Huu ulikuwa ni zaidi ya utafutaji. Kwanini wachangue hivi...? Niliwaza huku nikiitazama saa yangu. Ilikuwa ni saa nane sasa, sikuwa nimeambua kitu kwenye uchunguzi wangu kwenye nyumba hii ya Dokta Omary Maboli Siki hivyo nikatoka ndani humo na kuiacha kama ilivyo na kuelekea mahali ambapo niliegesha gari.




Muda mfupi baadaye nilikuwa mbali kabisa na nyumba hiyo nikikaribia kufika Sabasaba ambako ndiko nilikokuwa nikiishi. Nilipofika nyumbani kwangu sikuwa na fikra nyingine tena zadi ya kulala tu maana nilichoka sana na usingizi ulishaanza kunisumbua, niliegesha gari langu kwenye maegesho ya magari mara baada ya kulifungua lango la nyumba yangu sikuchelewa kutoka pia mvua ilishaanza kupunguza kasi hivyo nilitembea bila haraka hadi nilipofika barazani nikafungua mlango na kuingia ndani na kuufunga mlango huo nikaelekea chumbani kwangu baada ya kutazama hapa na pale. Nilivua nguo zangu zote na kujifunga upande wa Khanga nikajitupa kitandani bila hata kuoga.


Nilikuwa hoi kwa uchovu.




_________




Sikujua hata mvua ilikata saa ngapi kilichoniamsha ni kengele ya muda niliyokuwa nimeitega ili nisiweze kupitisha muda wangu wa kuamka, akili ilikuwa ikifanya kazi lakini macho yaligoma kufunguka kila kitu nilikuwa nikikifanya nikiwa nimefunga macho vivo hivyo kama kuzima kengele hiyo na kuitafuta simu yangu kwa kuipapasa. Niliipapasa simu yangu kwa muda mrefu bila mafanikio nikapiga kite cha uchovu kisha papaso hilo nikalihamishia mwilini mwangu kuanzia mapajani mwangu, niliyapapasa mapaja yangu mazuri yenye minofu na rangi nzuri bila kujali kama nilikuwa nikiyafunua kwa kuivuta Khanga yangu juu sikudumu sana nikahamia tumboni hadi kifuani ambako niliweka kituo, nilipenda sana kukipapasa kifua changu kwani kilikuwa kikinipa raha ya aina yake hasa nilipokuwa nikiipitisha mikono yangu juu yake, niliendelea na zoezi hilo huku miguu yangu ikiwa haitulii sehemu moja mithili ya niliyebanwa na haja ndogo niliziumauma kingo za midomo yangu kadiri zoezi hilo la kukipapasa kifua changu lilivyokuwa likiendelea. Simu pekee ndiyo ilifanikiwa kunizuia kufanya huo ujinga ambao sikujua nini hitimisho lake, nikayafungua macho yangu ambayo bado yalisumbuliwa na ukungu wa usingizi kisha nikatazama mahali simu hiyo ilipo. Nilijikuta nikikurupuka kutokea kitandani baada ya kujua kuwa simu ilikuwa kwenye meza ya kujipodolea nikamtazama mpigaji huku nikiwa na hakika kuwa ni lazima awe ni mwalimu Dao hakika nililenga.




"Hallow mkuu?" Nilianzisha maongezi simuni baada ya kuipokea na kuitupia sikioni.




"Habari za asubuhi Catherine?" Aliongea mwalimu Dao akiwa upande wa pili wa simu hiyo.




"Nimeamka mkuu na hivi punde ndiyo nimetoka kitandani.....!"




"Najua umeamshwa na hii simu Catherine hata hivyo si tatizo najua umefanya vema?" Aliifanya kauli yangu kuning'inia hewani mara baada ya kunikatisha. Nilijipa muda kidogo kabla sijajibu nikaishikilia nguo yangu vizuri kifuani kisha;




"Nimeifanya vema mkuu hakuna shaka na....!"




"....Ni vema ukawahi sasa ofisini utanikuta nikikusubiri isifike saa tatu..."




"Sawa mkuu." Nikamjibu kisha nikairudisha simu pale mezani na kujinyoosha kidogo kuuweka mwili sawa baada ya zoezi hilo nikaelekea Maliwato kwa ajili ya kupata huduma zote muhimu. Dakika thelathini zikatosha kumaliza haja zote na kurudi chumbani kwangu na kujiandaa, njaa ilianza kulisumbua tumbo langu maana sikukumbuka ni wakati gani nilitia kitu tumboni mwangu hata hivyo sikutaka kujisumbua kutaka kukumbuka kwani nilijipa hakika kubwa sana kuwa siku iliyopita ilikuwa ya kuhangaika sana hivyo hadi nakikurubia kitanda, tumbo langu halikuingiza kitu. Nikajiamuru kabla ya kitu chochote kwanza nitafute mahala pazuri nipate kifungua kinywa ndipo nielekee ofisini. Muda mfupi baadae nilishamaliza kujipodoa hivyo sikuwa na sababu za kuendelea kupoteza muda wangu, nilichukua simu yangu ya mkononi na kuitia kwenye mkoba huku nikihakikisha vitu vyote muhimu nimebeba. Nikatoka na kuchukua gari yangu nikaanza kuondoka maeneo hayo niishio hadi nilipofika barabara ya Sua nikaamua kuifuata hiyo kwa makusudi makubwa kabisa. Saa yangu ilikuwa ikiniambia kuwa kwa majira hayo ilikuwa ikikimbilia saa mbili na ushei, sikuwa na shaka ya kuwahi kwani mji huu wa Morogoro haukuwa na foleni za kuweza kuzuia au kuiwekea vikwazo vya mara kwa mara safari yangu. Mbele kidogo upande wa kulia niliona jengo nililolikusudia hasa kwa jambo nililotaka kulikamilisha kwanza, lilikuwa limeandikwa kwa maandishi makubwa KUDU'S REST HOUSE. Hapa niliamini ningeweza kupata huduma ya kulihudumia tumbo langu kwa vile hasa nitakavyo, nikaliingiza gari maegeshoni na kuteremka kisha nikaingia kwenye jengo hilo ambalo kwa majira hayo ya asubuhi kulikuwa na watu kadhaa waliokuwa wanaingia kwa ajili ya kupata chochote huku wengine wakiwa wanatoka.








Mbele kidogo upande wa kulia niliona jengo nililolikusudia hasa kwa jambo nililotaka kulikamilisha kwanza, lilikuwa limeandikwa kwa maandishi makubwa KUDU'S REST HOUSE. Hapa niliamini ningeweza kupata huduma ya kulihudumia tumbo langu kwa vile hasa nitakavyo, nikaliingiza gari maegeshoni na kuteremka kisha nikaingia kwenye jengo hilo ambalo kwa majira hayo ya asubuhi kulikuwa na watu kadhaa waliokuwa wanaingia kwa ajili ya kupata chochote huku wengine wakiwa wanatoka. Viti kadhaa vitupu vilikuwa vikinitazama huku vikitegemea kukaliwa nami kwa namna moja ama nyingine hata hivyo kati ya vyote nilivutiwa na kiti kimoja ambacho kilikuwa kimejitenga kidogo huku mbele ya kiti hicho kukiwa na meza ya plastiki ya rangi ya kibuluu ya sazi ya kati huku kukiwa hakuna kiti kingine zaidi ya hicho. Nikajivuta na kuketi muhudumu alipokuja nikaagiza kifungua kinywa kizito cha supu makini ya Sato, Chapati mbili imara na kikombe matata cha maziwa ya moto. Nilikula kwa haraka kidogo ili kuweza kuendana na muda lakini pia ulaji wangu ulidhihirisha njaa ambayo nilikuwa nayo sikujali, nilikula na muda mfupi baadaye nikawa nimekwisha maliza. Nililipa nilichotakiwa kulipa nikatoka hadi nje ambako kulikuwa na duka moja nikachukua chupa kubwa ya maji na kurudi garini.




Dakika tano mbele zikanikuta Rombo White Bar nikiwa naegesha gari langu. Nilijipa muda kwanza wa kulikagua eneo hilo kama kawaida yangu nilipojihakikishia kuwa hakukuwa na mabadiliko yoyote ndipo nililiacha gari langu hapo na kuzitupa hatua zangu taratibu. Nikiwa natembea kwa mwendo wangu wa kike wenye ukakamavu usiyojificha ama usiyoyaficha maungo yangu laini ya kike, fikra ya tukio la usiku likajijenga kichwani mwangu, taswira ya chumba cha Dokta Omary Maboli Siki kilivyochakuliwa kama kilichoingiliwa na mwendawazimu sugu wa Jaa kuu la jiji ikawa inausumbua sana ubongo wangu sikuwa na hakika kama katika upekuzi ule wapekuaji waliweza kutoka mikono mitupu.




Lazima kulikuwa na ulazima wa kutenda yale. Nilijipa hakika mwenyewe mawazoni. Nilichokuwa nikiwaza na kuwazuwa kwa wakati huo mmoja ni kwa vipi namna ya upekuwaji uwe tofauti? Hili ndilo hasa lililokuwa likinisumbua akili yangu hata hivyo sikuwa nimeweza kujipa majibu ya uhakika kwani pengine nyumba iliyopekuliwa ilikuwa ni moja na ya Dokta Lumoso ikawa haikuwahi kupekuliwa. Nikaliacha liliwe na kunguru wazo hilo. Nilizitupa hatua zangu kwa haraka sana huku sauti ya mgongano kati ya kiatu changu cha ngozi chenye soli ngumu na sakafu imara ya koridoni ikisikika vema. Sasa nilitazamana na mlango wa ofisi ya mwalimu Dao niligonga kwa utambulisho elewevu kisha nikasubiri kwa sekunde kadhaa tambulishi ndipo nilipousukuma mlango huo. Nilimkuta mwalimu Dao akiwa amejaa kitini mwake akinitazama katika namna ya mtu mwenye shauku kubwa ya kutaka kujua nini nilicho nacho, nikanyooka saluti kwa heshima, kama kawaida yake akaipokea kwa tabasamu kisha akanikaribisha kitini nami nikaketi. Kinywani mwake alikuwa amepachika mlingoti mpya kabisa wa sigara ambao alikuwa akiendelea kuuvuta taratibu.




"Catherine wa Catherine nini ulichoweza kupata kwenye hatua yako ya awali?" Akaniuliza baada ya kunitazama kwa kitambo kidogo akiwa anautafuna mlingoti wake wa sigara taratibu na kwa madaha makubwa. Nilijipa utulivu kabla ya kuamua kujibu nilichoulizwa baada ya kujihakikisha kuwa nimeweza kuvuta pumzi za kutosha ndipo nikamtazama usoni na kumwambia.




"Mkuu uchunguzi huu nimeweza kuufanya vizuri hata hivyo kuna mambo machache ambayo nimeweza kuyaona yakanichanganya kwa namna moja ama nyingine," nikaweka koma nikimtazama usoni kama ninayesoma taarifa fulani kwenye sura yake, akapeleka mlingoti wa sigara yake kinywani na kunitazama akitaka nizidi kumueleza.




"....Nyumba ya Dokta Omary Maboli Siki imefanyiwa upekuzi wa kina sana mkuu....!"




"Nadhani nilikuambia kuwa kuna wanausalama wapo kazini kwa amri ya Rais na kazi hiyo ikiongozwa na mkuu wa masuala ya upelelezi ndani ya usalama wa taifa Mwambije Mkami." Aliniambia mwalimu Dao huku akinitazama kwa mtazamo wa kiudadisi kama niweza kumuelewa.




"Inawezekana wakawa wamepekua nyumba ya Omary Maboli Siki pekee?" Nikamuuliza kwa shauku nikiwa na hamu ya kujua zaidi.




"Hapana kuna uwezekano mkubwa hiyo nyumba imepekuliwa hivi punde kwani mwanzo hazikuwa zimepekuliwa kwa namna hiyo unayoniambia, zilipekuliwa kitaalamu sana kwa hiyo kama umeweza kugundua nyumba ya Dokta Omary Siki imepekuliwa hivyo basi; wapekuwaji wangeweza kurudi kwa Dokta Lumoso tena...sasa nini umegundua?" Akaniuliza mwalimu Dao baada ya kunieleza hayo kwa uchache, akanitazama usoni huku akiipeleka sigara yake kinywani. Nilifungua mkoba wangu nikatoa ile redio kaseti ya zamani na kile kifaa kidogo kilichokuwa kimeunganishwa kwa uhodari mkubwa nikaviweka mezani. Mwalimu Dao alikuwa akivitazama vile vitu kwa udadisi sana nilitoa waya na kuunganisha kwenye umeme na kuiwasha ile redio umakini ukawekwa katika kusikiliza kilichopo redioni. Tulisikiliza kwa pamoja hadi pale ilipofika ukingoni. Sauti za kibabe kama; '....weka utulivu Dokta Lumoso Papi Mmbai...' Au ile ya kuuliza ya Dokta Lumoso kisha kibesi kusikika tena. '.....wewe ukifikiria unadhani tumekuja kufanya nini kwako...? Unadhani tumekuja kwa ajili ya kupata matibabu labda au......!'




Kila kitu kilisikika kwa uwazi kabisa na mwisho ndiyo ilikuwa imewaacha hoi. '....Musa anakuhitaji kwa udi na uvumba na ndiye aliyetutuma tukupeleke kwake...!'




Utulivu uliyeyuka kama siagi kwenye maji ya moto, nikamuona mwalimu Daniel Matia Okale akiuegamiza mgongo wake kitini na huku pumzi nyingi zikimtoka kifuani mwake akanitazama kwa sekunde mbili akageuza shingo yake pembeni na kutazamana na rafu ya vitabu. Alipopata utulivu ndipo akanitazama tena.




"Umeshajaribu kumfikiria mtu anayeitwa Musa?"




"Unadhani huyu Musa ni mtu?" Nikamuuliza huku nikilipuuza swali lake aliloniuliza, nilimuona akinikata jicho la mshtuko na kulivuta lile faili ambalo nililipata kwenye nyumba ya Dokta Lumoso Papi Mmbai kwa maelekezo ya ile redio kaseti. Akalifunua taratibu huku sigara akiwa ameibana kwenye kingo za mdomo wake ikiendelea kuungua taratibu. Akavuta pafu kubwa na kuishikilia kwa mkono wa kushoto huku sura akiwa ameikunja kwa namna ya kuuvuta moshi wa sigara ile kinywani mwake huku moshi mwembamba ukikatiza usoni mwake kwa namna ya kuiogelea anga na kumfanya kuyafinya macho yake katika namna ya kuifurahia ile burudani yenye madhara kabla hajaumwaga moshi mwingine mwingi toka kinywani.




"Unafikira tofauti kuhusiana na hilo neno Musa tofauti na maana yake halisi?" Akaniuliza huku akiwa ameelekeza macho yake kwenye lile faili akisoma baadhi ya maneno yaliyokuwa yamechapwa akiyaacha yale yenye hati ya mkono akiwa hajayaelewa. Nilimtazama usoni kwa udadisi akiwa anayasoma yale makaratasi baadhi.




"Hata kama nitakuwa na hisia tofauti bado utakuwa ni mtihani kupata majibu elewevu, linanichanganya." Nilimjibu nikiwa namtazama bado. Mh! Akaguna. Na kufunika lile faili akaipeleka sigara yake kinywani na kuivuta tena kisha akakung'uta majivu kwenye kikombe kile cha majivu.




"Nini mkuu?" Nikamuuliza.




"Hizi karatasi zilizo chapwa umezisoma?" Akaniuliza sasa akinitazama usoni. Nikaiona sura yake ilivyojikunja na kuweka makunyazi ya kizee kwenye paji lake la uso.




"Nilizisoma lakini hazikunipa majibu niyatakayo niliona ni maelezo ya kuichunguzi ya ugonjwa wa Kansa ya Damu lakini sidhani kama lina mashiko sana hadi kuweza kulificha kwa kiasi kikubwa namna hii." Nilimjibu kisha nikafungua mkoba wangu na kutoa PK fresh na kuanza kutafuna taratibu baada ya kuimenya na kutupia tembe mbili kinywani huku nyingine mbili nizirudisha mfukoni zikiwa kwenye karatasi yake. Nilimuona Daniel Matia Okale akinitazama kwa kina kisha akaibana kwa mara nyingine sigara yake kwenye kingo za midomo na kuivuta kwa nguvu na kukitupia kipisi kwenye kikombe kile kigumu cha majivu.




"Kuna kubwa liko hapa Catherine na nina mashaka na hii hati ya mkono siamini na kujipa uhakika eti, haina maana hii na kama kweli ingekuwa haina maana isingeweza kufichwa na kuamua kutoa maelezo ya mahali alipokuwa amelificha hili faili. Huwenda hili likatujulisha mahali ambako amepelekwa." Akaweka tuo mwalimu Dao kisha akanitazama tena usoni kwa tuo aliporidhika na muda wake wa kupumzika akaendelea.




".....lazima hii hati ya mkono tuijue inamaanisha nini na kwanini hati yake iwe imeandikwa kwa maandishi ya kidaktari. Nenda Hospitali ya mkoa ukifika muulizie Daktari Gabriel Nyagile kisha kabla hujampa hili faili mwambie nimeagizwa na Daniel Matia Okale atakuwa radhi kukusikiliza shida yako." Akaniambia mwalimu Dao kisha akaachia tabasamu la matumaini kuhusiana na jambo hilo nami nikalichukua lile faili huku ile redio kaseti akiichukua yeye na kuitafutia mahali pa kuiweka. Nililitia kwenye mkoba wangu lile faili na kunyanyuka kutokea pale kitini na kupiga saluti akaijibu kisha nikarusha hatua kuukabili mlango.




"Utayaleta majibu kwenye ofisi kubwa kitengoni," aliniambia nikatikisa kichwa kuafiki huku nikitoka na mlango ukijifunga nyuma yangu. Nilikuwa na ari ya kazi sasa na hadi hapa nilikuwa kwenye kazi rasmi, moyo wangu ulikuwa ukisukuma damu kwa kasi sana kwani hata mapigo yangu ya moyo yalikuwa kwenye kasi sana kijasho kilianza kunitoka kutokea sehemu mbalimbali za mwili wangu. Nilikuwa nikiipita Hoteli ya Mt. Uluguru nikaongeza kasi ya gari langu hadi nilipoikuta barabara ya Madaraka nikaifuata kwa upande wangu wa kulia baada ya kusubiri magari matatu yanipite nikaendesha taratibu kutokana na gari zilizonitangulia kuwa katika mwendo wa taratibu kuku upande wa kulia kukiwa na gari zilizotokea mjini hivyo kuninyima nafasi ya ku-ova teki. Niliipita Muradds Mini Supermarket nikafanikiwa kuyapita magari yaliyoko mbele yangu kisha nikaipita tena Benki ya Barclays kisha kituo cha mafuta cha Oil Com nikiwa kwenye barabara ya Old Dar es salaam nikaendesha gari kidogo kwa mwendo mchache nikaingia kulia nikaja kuegesha gari langu kwenye viunga vya Hospitali kubwa ya rufani ya manispaa ya Morogoro. Kwa kuwa niliegesha gari langu upande wa pili wa barabara nilisubiri kwanza gari lipite kisha pikipiki ndipo nikafungua mlango na kutoka nikavuka barabara na kulielekea lango la kuingilia hospitalini hapo. Ilikuwa ikikimbilia saa nne na ushei hata hivyo sikuhofia kuingia langoni hata kama haukuwa muda wa kuwaona wagonjwa. Niliwaeleza walinzi shida yangu ikiwa ni pamoja na kujitambulisha kwa uongo mwingi.






Kwa kuwa niliegesha gari langu upande wa pili wa barabara nilisubiri kwanza gari lipite kisha pikipiki ndipo nikafungua mlango na kutoka nikavuka barabara na kulielekea lango la kuingilia hospitalini hapo. Ilikuwa ikikimbilia saa nne na ushei hata hivyo sikuhofia kuingia langoni hata kama haukuwa muda wa kuwaona wagonjwa. Niliwaeleza walinzi shida yangu ikiwa ni pamoja na kujitambulisha kwa uongo mwingi.


Wakaniruhusu.




Niliufuata ujia mwembamba ambao ulinipeleka hadi kwenye wodi za wanawake hapa nikasimama baada ya mbele yangu kumuona muuguzi akija upande wangu akionekana kuwa na haraka kidogo. Alivaa gauni la moja kwa moja la rangi nyeupe ambalo lilikuwa limeyavuka magoti yake kidogo tu huku mikononi akiwa amevaa glovu za mipira.




"Habari yako dada?" Nilimsalimia nikiwa nimeweka tabasamu la kirafiki.




"Salama tu vipi?" Alinijibu akinitazama huku usoni kwake akiwa hana tabasamu sana labda ni kutokana na ubize aliyojivika nao.




"Samahani kwa kukusimamisha hapa najua uko na majukumu dada yangu," nilimuomba baada ya kumuona akiwa na mashaka hata hivyo alinitazama kwa kunishangaa maana sikuwa na tashwishi yoyote usoni mwangu zaidi nilimpa tabasamu.




"Ooh! Bila samahani nakusikiliza." Akanijibu huku akiachia tabasamu na yeye hapa nikaukadiria umri wake kupitia sura yake alikuwa akikimbilia miaka ishirini na sita na saba alikuwa na umbo zuri la kike lililojitenga huku nyonga yake ikijidhihiri waziwazi na mzigo ulioko nyuma ya mgongo wa dada huyo. Sura ya duara iliyobeba macho madogo kiasi yaliyopakwa wanja kileo zaidi na midomo iliyopakwa rangi nyekundu vikamfanya kuwa kwenye daraja fulani la wanawake wachache warembo.




"Nina shida na Dokta Gabriel Nyagile?" Nikaweka ombi langu huku nikiendelea kutabasamu na kuzidi kuitafuna PK yangu fresh ambayo niliibakisha. Akanitazama kidogo kisha akaniambia nimfuate. Nilipokuwa nyuma ndipo nikagundua madini aliyoyabeba nyuma ya mgongo na yalikuwa madini kweli maana hata akitembea hakuwa akiyalazimisha yatikisike kama wengine wafanyavyo bali haya yalikuwa yakitikisika yenyewe. Alikuwa mfupi kiasi mwenye umbo la wastani. Kwa mtazamo huu huwezi kubisha kuwa huyu alizaliwa Morogoro tena akiwa ni Mluguru wa pande zote mbili baba na mama hata hivyo ningeweza kusema alikuwa ni mingoni mwa waluguru warembo kuliko wote niliyowahi kuwaona. Tukiwa tunatembea kwa mwendo wa haraka kidogo, tukaingia mlango huu na ule lakini njiani tukapunguza mwendo baada ya yule muuguzi kusimama mbele ya mzee mmoja aliye katika koti refu la kidaktari na kifaa cha kupimia mwenendo wa mapigo ya moyo ya binadamu kikiwa kinaning'inia shingoni huku ile sehemu ya kupachika masikioni ikiwa imeingia kwenye mfuko wake wa koti la kidaktari uliyopo kifuani upande wa kshoto. Kwa tathmini ya haraka alikuwa akikimbiza umri wa miaka hamsini hamsini na tano hivi na kidogo. Alivaa miwani ya macho kichwani akiwa na upara katikati na nywele chache nyeupe zilizopitishiwa kitana vizuri zikiwa zimepita pembeni kukizunguuka kile kipara alionekana kuwa ni mwenye tabasamu muda wote. Yule Nesi alisalimiana na yule Daktari kisha kumuelekezea kwangu kama mgeni wake. Mzee yule alinitazama lakini hakuonesha kukumbuka chochote kama alishawahi kuniona mahali. Yule Nesi alinigeukia na kunitazama kisha akasema;




"Dada huyu mtu uliyekuwa ukimuulizia," nikamshukuru kisha akaondoka. Mbele yangu nilitazamana na Daktari yule mzee nikampa mkono nikiwa kwenye Tabasamu naye akaupokea akilirejesha tabasamu la kirafiki.




"Naitwa Catherine!" Nilijitambulisha baada ya kuuachia mkono wake.




"Naitwa Dokta Gabriel Nyagile karibu?" Naye alijitambulisha huku akiwa bado kwenye tabasamu.




"Asante Daktari Gabriel Nyagile, nadhani tungepata sehemu tulivu kama huto jali," niliitikia ukaribisho na kutupia ombi langu. Nilimuona akinyanyua mkono uliobeba saa kisha akanitazama.




"Japo sina muda sana maana nilikuwa naelekea kupata chakula mjini."




"Unausafiri?" Nilimuuliza.




"Hapana sikuja na usafiri hata hivyo nitatumia mwendo wa miguu maana ni moja ya mazoezi si unaona umri wenyewe!"




"Hakika lakini hata mimi nikitoka kwako ni safari ya huko huko mjini hivyo si vibaya tukiongozana na tungeweza kuzungumza tukiwa garini?" Nilimwambia nikiwa nimechanua tabasamu kama ada, akanitazama kidogo kisha akataka kusema jambo akasita. Akageuka pembeni baada ya kuitwa na kijana mmoja aliyevalia kitabibu kama yeye wakasalimiana kisha kijana yule akaondoka akageuza macho yake kwangu akanitazama tena.




"Nifuate ofisini naweza kukusikiliza kwa utulivu zaidi." Akakata shauri. Tuliongozana na kutoka nje ya ile wodi ya wagonjwa wa matumbo tukaingia kwenye wodi nyingine ya watoto tulipotokea kwenye mlango mwingine tukavuka nyasi fupifupi na kuifuata baraza ndefu na kukunja kushoto tukaingia kwenye chumba kimoja kitulivu ambacho kilikuwa ni cha katibu muhtasi maana niliona mashine ya kuchapa, tarakilishi ya kizamani na mashine nyinenyingine tukaingia kwenye chumba kingine hapa tulikaribishwa na hewa safi ya kiyoyozi kilichokuwa kikifanya kazi muda wote. Dokta Gabriel akakitoa kile kifaa cha kupimia mwenendo wa mapigo ya moyo na kukipachika mahali kisha akalivua koti lake la kidaktari na kulitindika kwenye enga mule ndani akabakiwa na shati la mirabamiraba alilolichomekea huku chini akiwa amevaa suruali nyeusi ya Tatroni ambayo haikunyooshwa vema lakini haikuwa ikijulisha alikuwa ameufunga mkanda wake wa ngozi barabara uliyoikamata suruali yake vizuri na kumchora kitambi cha wastani kilichoshindwa kujificha. Akazunguka nyuma ya kiti chake na kabla ya kukaa akageuka na kunitazama kwa muda mfupi, hakusema kitu akakaa kitini nyuma ya meza yake ya ofisi ambayo ilibeba mafaili kadhaa ya kazi, baadhi ya chupa ndogo za dawa, pakiti chache za vidonge ambavyo mara baada ya kukaa alizichukua na kuzitumbukiza kwenye kiboksi kidogo akakifunga na kukitupia kwenye boksi kubwa la wazi lililopo mbele upande wa kulia karibu na rafu kubwa ya vitabu vya kitabibu na mafaili mengi yaliyopangiliwa vema. Kulikuwa na friji dogo ambalo lilikuwa na shughuli ya kupoza maji tu pekee lakini pia kulikuwa na kitabu kikubwa cha kibaolojia pembeni ya ile meza upande wake wa kushoto. Macho yangu yaliporidhika na utalii ule nikayarudisha kwa yule mzee naye akanitazama huku akinitaka nikae. Nikavuta kiti na kuketi. Dokta Gabriel Nyagile alivuta mtoto wa meza na kutoa pakiti ya sigara 'SM' ambayo ilikuwa mpya kabisa akaichana kidogo kisha akaipiga kwa matumbo yake ya vidole viwili sigara kadhaa zikajitokeza. Akailekezea kwangu ile pakiti nami sikumuangusha nikachomoa moja na kuipachika kwenye kingo za midomo yangu nilipotazama upande wangu wa kulia pale mezani niliona kiberiti cha gesi chekundu chenye lebo ya BiC. Nikailipua sigara yangu na kwa msaa wa kiberiti hichohicho nikaiwasha sigara yake iliyopo kinywani mwake, nilimuona Dokta Gabriel Nyagile akiuvuta moshi kwa nguvu sana mapafuni mwake huku akijilaza kwenye kiti chake cha kiofisi akinitazama sambamba na kuutoa moshi kinywani mwake pembeni. Alionekana kuwa na uchu sana na Sigara ile.




"Huwa napenda kujiburudisha kwa kilevi hiki kilichoiteka akili yangu hata kunizuia nisioe....nikiwa na kiburudisho hiki huwa najiona niko salama na mzima kiakili napenda kujiliwaza nacho hasa nikiwa nimemaliza baadhi ya majukumu yangu." Alisema Dokta Gabriel Nyagile kisha kabla sijajibu kitu akashtuka, nafikiri kumbukumbu za uwepo wangu mbele yake ulimrudishia akili yake upya akanyanyua mgongo wake na kunitazama usoni kwa makini huku ike tashwishi iliyokuwa ipo hapo awali akiwa ameiondosha usoni mwake.




"Catherine si ndiyo?" Akaniuliza. Nikatikisa kichwa kukubali huku nikivuta ile sigara kwa pozi la kutokuwa na haraka.




"Naweza kukusikiliza shida yako sasa!" Akaniambia huku akiweka umakini machoni mwangu, nilimtazama kwa sekunde kadhaa kisha nikachukua mkoba wangu na kufungua na kutoa lile faili nikalitupia mezani. Nikamuona akilitazama kwa udadisi huku akiipeleka sigara yake kinywani na kuivuta bila kujali maandishi ya onyo yaliyoandikwa kwenye ile pakiti ya sigara ambayo yalikuwa yakinadi kuhusu uhatari wa kuvuta sigara bila shaka yale maandishi aliyabadilishia maana badala ya 'uvutaji wa sigara ni hatari kwa afya yako' yeye aliyalazimishia maana na kuyapa maana mpya ya 'uvutaji wa sigara ni tulizo la mawazo yako'. Alinitazama usoni baada ya kuliangalia nikampa ishara alifunue kabla ya kulifunua nilimuona akianza kuwa na wasiwasi kidogo. Akalifunua na kuanza kulipitishia macho nilikuwa nikimuangalia usoni kwa udadisi mkubwa sana hadi kufanikiwa kuuona mshtuko uliyompata kwa kiasi fulani.




"Umeweza kugundua kitu Dokta?" Nilimuuliza lakini hakunijibu aliendele kulifunua na kulipitishia macho kisha nikamuona akipumua kwa nguvu akatoa miwani yake ya kusomea machoni akaipuliza kidogo akiwa ameachama kinywa katika hali ya kupata unyevunyevu kisha akaipitisha kwenye shati lake akiifuta na kuirudisha machoni akaivuta sigara yake na kutoa moshi mwingi nje kisha akairudisha tena kinywani akaibana na kingo za midomo yake akaiacha hapo ikiteketea taratibu.




Nilikuwa nikiivuta sigara yangu huku nikimtazama bila wasiwasi wowote nilimuona jinsi alivyokumbwa na wahaka mkubwa sana. Akayapitia yote kisha akanyanyua macho yake na kunitazama.




"Hili faili umelitoa wapi binti?" Aliniuliza baada ya kumaliza kulipitishia macho. Sikuwa mkurupukaji katika kujibu nilipenda kuwa makini sana hasa niwapo kwenye kazi muhimu kama hii, nilijisawazisha pale kitini na kumtazama.




"Umeweza kulijua ni la nani au linatoka wapi?" Nilimuuliza nikijua ni lazima ajigonge katika kujibu. Nikaendelea kuivuta sigara yangu huku nikimtazama usoni. Dokta Gabriel Nyagile akatulia akiwa kama anayevuta tafakuri fulani kichwani mwake utulivu ukaiba muda wa mahala hapo kidogo na kuchukua mamlaka kwa kiasi fulani.






"Umeweza kulijua ni la nani au linatoka wapi?" Nilimuuliza nikijua ni lazima ajigonge katika kujibu. Nikaendelea kuivuta sigara yangu huku nikimtazama usoni. Dokta Gabriel Nyagile akatulia akiwa kama anayevuta tafakuri fulani kichwani mwake utulivu ukaiba muda wa mahala hapo kidogo na kuchukua mamlaka kwa kiasi fulani.




"Wewe ni nani kwani?" Akaniuliza huku lile swali langu akilipuuza kama nilivyolipuuza la kwake, akili yangu ikafanya kazi ya haraka ya kujua ipo namna katika kupata kitu kwa mtu huyu hivyo kwa haraka nikatoa kitambulisho changu cha kazi na kumpatia Daktari huyo. Kilikuwa ni kitambulisho halisi na sikuona sababu ya kumdanganya.




"Nilijua tu wewe utakuwa ni mwanausalama, mpelelezi; sasa kwanini unachunguza maisha aliyokuwa akiishi Dokta Lumoso Papi Mmbai?" Akaongea kabla ya kuniuliza na hata nilipomjibu hakuwa tayari kunieleza nilichokitaka. Nikaanza kuingiwa na wasiwasi na nikaona huwenda nisingepata ninachokitaka kwa uwazi zaidi hivyo nikaamua kujitambulisha kama mkuu wangu alivyoniagiza. Nikamwambia kuwa nimeagizwa na mwalimu Daniel Matia Okale. Nilimuona akinitazama vizuri kisha akatengeza uso kwa tabasamu la kuonesha matumaini huku bilashaka akili yake ikiwa huru kuongea na mimi.




"Ohoo! Kumbe umeagizwa na patna? Hakuna shaka kwake sina ajizi nitakuwa huru kukujibu chochote sasa." Akaniambia. Nikatabasamu naye akatabasamu kuonesha kuwa tuko pamoja.




"Ametaka hili jambo liwe siri sana, siri sana kwani hupaswi kumuamini mtu." Nikamwambia hata hivyo alinitazama kwa wasiwasi na kuonesha mashaka juu yangu huwenda alikuwa bado haamini kama nilitumwa kweli na Dao ingawa hakuwa na namna zaidi ya kuniuliza lile swali lake lisilojibiwa huku sura yake ikiwa haiko sawa.




"Hapana sichunguzi maisha aliyokuwa akiishi Dokta Lumoso namna tofauti kwani hujui kuwa Dokta Lumoso Papi na Dokta Omary Maboli walipotea kwenye mazingira ya kutatanisha?" Nilimjibu kisha nikimuuliza swali, nilimrudisha kwenye ile hali ya kawaida baada ya kujua kuwa mimi sikuwa mtu mbaya kwake. Akaivuta sigara yake kisha akasema.




"Najua na ilikuwa ni ajabu sana kutekwa kwao ama kupotea kwao kwa kweli hadi sasa siamini kama watu muhimu kama wale waliyokuwa na mchango mkubwa nchini wapotee hivihivi halafu serikali ikae kimya."




"Ngoja Dokta, kwani kabla ya kupotea hawa madaktari, uliwahi kuzungumza nao kwa mara ya mwisho au mlikuwa na ukaribu wa kiasi gani?"




"Unajua ni miaka mingi sana karibia miaka ishirini na kitu sasa kama sikosei nadhani!"




"Najua lakini sidhani kama kumbukumbu zinaweza kupotea?" Nilimuuza huku nikimtazama usoni. Nilimuona akifikiri kwa kitambo kidogo kabla ya kunijibu, aliyazungusha macho yake kutokea kulia kwenda kusho, juu chini kisha akajiweka vizuri kitini.




"Kuhusu Dokta Lumoso Papi Mmbai sikumbuki lakini Dokta Omary Maboli Siki nakumbuka tena nakumbuka vizuri sana. Ilikuwa ni siku moja kabla ya kupotea kwake....si unajua kuwa walipotea siku moja....? Nilikutana naye mahali nafikiri ni kwenye burudani kama sikosei tulikuwa kwenye ukumbi wa Morogoro Hoteli tukiwa tumeitika mualiko wa harusi ya rafiki yetu, baada ya burudani kwisha na kufikia muda wa kupata chakula ndipo Maboli aliponifinya sikio na kunitaka tuwe faragha kidogo. Tukachukua chakula na kwenda kutafuta mahala tulivu na kunielezea kwa uchache wasiwasi wake. Kikubwa alichozungumza na ninachokikumbuka hadi leo ni kupokea maneno ya vitisho kutoka kwa watu wasiyojulikana. Alinitaka ushauri kuhusiana na hofu ile iliyomkumba, sikuwa najua kama alikuwa anamaanisha hasa kile akisemacho kwani mtu yule alipenda sana masikhara hivyo nilijua ni miongoni mwa masikhara yake hata hivyo niliweza kumshauri juu ya kutoa taarifa mahali husika ili kuweza kuhakikishiwa usalama wake...!"




"....Alifanya hivyo...?" Nilimkata kauli na kumuuliza kama Dokta Omary alijaribu kutoa taarifa polisi au kwenye chombo chochote cha usalama.




"Muda, tatizo muda wa kufanya hivyo ndiyo haukuwepo kwani siku ya pili yake baada ya kuachana pale usiku ule, taarifa ambazo zilianza kuvuma kama utani zikasambaa kuwa Dokta Omary Maboli Siki na Dokta Lumoso Papi Mmbai hawaonekani. Zilichukuliwa kama utani lakini hatimaye siku zikakatika huku watu hao wakiwa wamepotea kweli hata wanausalama walipokuja kuanza msako wa kuwatafuta ilikuwa kazi bure kabisa hatimaye watu wakasahau huku mioyo ya ndugu zao pekee ndiyo ikibaki na maumivu." Akasema Dokta Gabriel Nyagile kisha akaiweka sigara kwenye kingo za midomo yake na kuivuta taratibu. Nilimuona akiwa amenyongea sana na hata uvutaji wa sigara yake ulikuwa kwenye mafikirio sana huwenda kumbukumbu hii ilimuumiza mno mzee huyo.




"Katika maelezo aliyowahi kukupa hakuwahi kukuambia kuwa hao waliyokuwa wakimpa vitisho walikuwa wakitaka nini hasa kwao au kwake?" Nilimuuliza huku nikijitahidi kumtazama katika namna ya kumtia moyo.




"Alisema kuwa alikuwa akiambiwa kuwa anahitajika na Musa....!"




"Musa....?" Nilishtuka baada ya kusikia jina hilo musa. Nikapata picha kuwa inawezekana wote wawili walipelekwa sehemu moja ila ugumu uliopo ni je, nani ni Musa na kwanini aliwataka madaktari wataalamu wote wawili? Cha ajabu ni kwamba wote taaluma zao zilikuwa zikiendana japo kila mmoja alikuwa na kitengo chake maalumu sasa iweje wote wachukuliwe. Hili likaniumiza sana kichwa na kila nilivyotafuta namna ya kufanya nilijikuta nikigonga ukingoni mwa fikra zangu. Nilitakiwa kumfahamu huyo Musa mapema sana kabla sijaamua kitu kingine.




*_______*




Mawazo yalinizonga sana kwa kweli lakini sikuona haja ya kuendelea kuwaza kwa namna moja ama nyingine nilichokifanya ni kuweka utulivu zaidi ili kupata fumbuo nikazirudisha kumbukumbu zangu mahala salama kisha nikamtazama Dokta Gabriel na kuitazama saa yangu, muda ulikuwa ukikimbia na nilikuwa nikiharibu muda wa Dokta Gabriel kupata chakula kwa mazoea ya ratiba yake ya kila siku ingawa nilimtaka radhi.




"Turudi kwenye hili faili sasa Dokta, kuna chochote umeng'amua hapa?" Nilimuuliza Dokta Gabriel Nyagile huku nikimuona akiutafuta utulivu fikrani mwake ili aweze kupata kitu. Alilitazama lile faili kwa macho ya haraka kisha akanitazama usoni.




"Haya maandishi yote kuanzia yaliyo chapwa hadi hii hati ya mkono ni uchunguzi wa ugonjwa hatari sana na ugonjwa huo ni saratani ya Ubongo...!"




"Najua Dokta kuwa hizi karatasi zilizochapwa zimebeba uchunguzi tiba wa saratani ya Ubongo wasiwasi wangu ni kuhusiana na hii hati ya mkono nayo inazungumzia jambo hili hili moja?" Nilimkatisha Dokta Gabriel nikimuuliza kuhusiana na nikijuacho.




"Ndiyo, vyote vinazungumzia kitu kimoja." Alinijibu akiwa katika utulivu sana.




"Kwanini viwe katika namna tofauti ya kiuandishi?"




"Nilikuwa naendelea ili nifike kwenye wasiwasi wako," akasema na kuweka koma kisha akavuta sigara yake na kulivuta karibu lile faili na kulipitishia macho kwa jozi ya sekunde akasema.




"Hii hati ya mkono iliuzungumzia ugonjwa wa saratani ya Ubongo kwa undani zaidi kuanzia namna unavyoibuka kwa mgonjwa nikiwa na maana jinsi unavyoanza kumkumba mgonjwa, viashiria vya ugonjwa wenyewe na udhibiti namna tiba inavyopatikana kwa mgonjwa wa saratani ya Ubongo."




"Unaweza kufikiria labda ni kwanini aliamua kufanya uchunguzi huu kwa kina namna hii na akaweka rekodi kabisa kama ushahidi? Pengine huu ulikuwa ni mpango ambao ulianza mapema au ni nini?" Nilimuuliza baada ya kunieleza kilichomo kwenye ile hati ya mkono nilidhani huwenda alianza kuchagizwa na maswali yangu ila sikujishughulisha kujali.




"Kama nilivyo wahi kukueleza kilichomkuta Dokta Omary Maboli Siki basi huwenda hata huyu vivo hivyo kwani hata ukiangalia upoteaji wao ulikuwa ni wa siku moja." Alinijibu. Nikaivuta sigara yangu kwa nguvu sana huku nikiurudisha mgongo wangu nyuma na kuukutanisha na foronya laini ya kiti kile iliyonipokea kwa ukarimu na kukifanya kichwa changu kiingie kwenye tafakuri ndogo. Nilifikiri kwa muda mdogo kisha nikaivuta tena ile sigara na kuutoa moshi kwa pembeni ya kinywa changu nikiilaza mikono yangu mezani nikimtazama kwa ukaribu daktari huyo mzee ambaye kwa makadirio ya umri wake wa miaka hamsini na tano hamsini na sita aonekane bado yuko fiti kiasi hata hivyo sigara zilionekana kumchosha zaidi lakini alikuwa imara bado na bila shaka serikali ilimnyima ustaafu makusudi kutokana na uwezo wake mkubwa kwenye anga ya utabibu aliyotunukiwa na Mungu.




"Hatuwezi kujua angalau chochote au popote walipopelekwa hawa watu?" Nikamuuliza nikiwa namtazama. Alinitazama kwa wasiwasi kwa kuwa swali nililomuuliza halikuwa chini yake hata hivyo nililiuliza kama mtego kwake na nikamuona akijiweka sawa.




"Kulikuwa na mtu mmoja aliyefahamika kwa jina moja la Mkude huyu bwana sidhani kama hadi sasa yuko hai maana ni muda mrefu kidogo sikupata kumtia machoni. Huyu bwana alikuwa na ukaribu mno na Dokta Lumoso Papi Mmbai ni kama kidole na ukucha au sime na Morani, sasa nina uhakika wa asilimia hamsini na kitu kuwa huyu bwana ni lazima atakuwa ameachiwa baadhi ya taarifa kama ungefanikiwa kumpata huyu ungepata mwangaza wa...!" Alikatisha kauli yake mara baada ya kukutwa na muayo mrefu wa njaa uliyochanganyikana na uchovu. Nikajua nimeutumia muda mwingi wa Daktari huyo pasipo kumpa nafasi ya kwenda kutia kitu tumboni mwake na sikuwa na uhakika kama asubuhi alitia kitu kizito. Niliitazama saa yangu hakika muda ulikuwa ukikimbia sana ilikuwa ikikimbilia saa nane.




"Naomba nisizidi kuupoteza muda wako sana mzee wangu labda kwa kunielekeza tu, huyo Mkude naweza kumpatia wapi?" Nilimuuliza hata hivyo hakuwahi kunijibu na badala yake alikuwa akiendelea kulifunua lile faili taratibu huku akiwa anatoa sauti ndogo ya kuunguruma iliyoashiria uchovu kiasi, sigara akiwa ameibana kwenye kingo za midomo yake. Niliendele kumtazama hivyo huku nikiuvuta moshi wa sigara ndani baada ya kutoka kuivuta punde. Hakika nilijikuta nikikumbuka enzi zangu nilipokuwa mvutaji mzuri wa sigara nikiwa shimoni nchini Marekani ikiwa ni sehemu ya kupambana na baridi. Nikiwa naifurahia ladha ya sigara ile nikamuona Dokta Gabriel akiiweka sawa miwani yake kisha akaliinamia lile faili vizuri akanyanyua sura yake na kunitazama tabasamu likimeremeta usoni mwake kama bwana harusi akabidhiwaye mke. Akapumua kwa nguvu kabisa na kukitupia kipisi cha sigara yake kwenye kile kikombe kigumu baada ya kipisi kile cha sigara kutaka kuanza kuziunguza kingo za kinywa chake.




"Mkude anapatikana Chamwino nitakupa maelekezo yote ila hebu tazama hapo chini kwenye hilo neno 'MUSA' kuna maandishi madogo ya hati ya mkono sijaelewa vizuri kutokana na macho yangu kuanza kukumbwa na ukungu wa uoni huwenda kwa macho yako unaweza kugundua kitu." Alinigeuzia lile faili Dokta Gabriel, nililisogeza kwangu na kulitazama kwa ukaribu na umakini wa hali ya juu sana. Naam! Niliona kitu na hiki kikanipelekea nikumbuke maneno ya mwalimu Dao mara baada ya kuniambia kuwa safari hii mimi ndiye nitakayekwenda Ungamo. Chini ya neno 'MUSA' kulikuwa na maandishi madogo yaliyokuwa yakisomeka kwa shida kidogo. 'Ungamo'. Ilinishtua moyo wangu kwa kiasi fulani na kuzipeleka fikra zangu maili kadhaa nilifikiri mengi hasa yale yote yaliyotiririshwa na fikra zangu ubongoni hatima ya yote nilivamiwa na tabasamu mara baada ya kujipongeza nafsini kuhusiana na mwenendo mzima wa upelelezi wangu. Nikamfikiria Dokta Lumoso kwa upana wake na kujiuliza alikuwa ni mtu wa namna gani mwenye uwezo mkubwa wa kufanya vitu vikubwa kama hivi ambavyo kwa namna moja ama nyingine vinaweza kuwa njia. Huwenda kuna vitu alivipata kutoka kwa watekaji na hakuona sababu ya kuvipuuzia. Haikuwa safari ndogo nikiri hata hivyo angalau nilifika kwenye mwangaza wa wigo uliofumbwa na Daktari Lumoso Papi Mmbai ili kuweza angala kupata msaada. Nikiwa najipumbaza kwa hili na lile nilimuona Dokta Gabriel Nyagile akiangalia muda kupitia saa yake ya mkononi, sikungoja kuambiwa kuwa sasa hakutaka mjadala mwingine alitaka kulihudumia tumbo lake na si vinginevyo.










Haikuwa safari ndogo nikiri hata hivyo angalau nilifika kwenye mwangaza wa wigo uliofumbwa na Daktari Lumoso Papi Mmbai ili kuweza angala kupata msaada. Nikiwa najipumbaza kwa hili na lile nilimuona Dokta Gabriel Nyagile akiangalia muda kupitia saa yake ya mkononi, sikungoja kuambiwa kuwa sasa hakutaka mjadala mwingine alitaka kulihudumia tumbo lake na si vinginevyo. Nilikusanya vyangu na kuvirudisha kwenye mkoba huku nikiwa na uhakika kuwa kazi ya hapa nchini imekwisha kilichobakia ni kuelekea Ungamo ambako matabibu hao wamesombelewa huko. Nilimpa mkono na kumshukuru kwa msaada mkubwa aliyonipatia pia nilimuomba radhi kwa kuubaka muda wake bila huruma na kulifanya tumbo lake lisilo na misuli imara ya kuvumilia njaa lineng'eneke pengine hata kunilaani kwa kitendo hicho cha kutojali wasaa wa mtu na ratiba zake. Alinipa maelekezo ya mahali ambapo ningeweza kumpata mtu anayefahamika kama Mkude kisha akaniambia.




"Usijali kuhusu hilo binti yangu niseme tu kuwa muda na wakati wowote utakapopata jambo la kunitaka msaada, wewe nikaribie tu nami sitosita kukupa nikijuacho. Daniel Matia Okale ni suhuba wangu wa muda mrefu sana hivyo nisingeweza kuacha kumsaidia kwa kile nikijuacho." Aliniambia nami nikamshukuru kwa jambo hilo hata hivyo kabla ya kuamua kuipa jukumu miguu yangu kunitoa mule ndani nilimtazama usoni kwa namna ya pekee kisha nikamuonya juu ya usalama wake na usalama wa kazi hii kwa ujumla. Ni lazima ahakikishe hatoi siri yoyote kuhusiana na ujio wangu mahala hapo aliponielewa japo bado sura yake ilikuwa na wasiwasi kama kweli mimi nilitumwa na Dao. Akili yake ilikataa na alikuwa na hofu isiyojificha ila nisingeweza kuiondoa hofu ile zaidi ya kuondoka, nilianza kupiga hatua zangu taratibu nikijitoa ofisini mwake huku nikiamini kuwa ni lazima atakuwa ananitazama hadi nilipokuwa nje ya ofisi yake.




*________*




Nilikuwa garini kichwa kikiwa na mawazo lukuki niliwaza mengi sana kuhusiana na mchakato mzima wa shughuli hii ilivyo ya ajabu na ambavyo ilihitaji akili nyingi kuifumbua. Pamoja na kwamba Dokta Lumoso Papi Mmbai alifanya haya akiwa na makusudi maalumu ya kutaka kupata msaada hata hivyo muda haukuwa sawia hata kidogo kwani ni takribani miaka ishirini ilishakatika msaada huu utakuwa wa namna gani sasa? Hili liliniumiza sana kichwa na kunisababishia shida ubongoni mwangu nilihisi kuchanganyikiwa kwa hali hii kwa kweli. Wakati nikiwa nawaza hilo nikalikumbuka lile faili ambalo ndilo lilinifanya kwa wakati huo kuyajua yote haya, akili yangu ikazama ndani kabisa ya fikra zangu sasa nikajua fika kuwa jambo hili lilikuwa katika mpango, tena mpango huu ni mpango kabambe. Nilifikiri kuhusiana na utafiti au uchunguzi wa ugonjwa wa saratani ya Ubongo ambao maelezo yake yalinipelekea nifike kwa Dokta Gabriel. Sasa nilikuwa naipita Benki ya CRDB kukikaribia kituo cha daladala kabla ya kuvuka kidaraja kidogo nikiiacha njia iliyokuwa ikielekea kituo kikuu cha Polisi Morogoro na uwanja wa Jamhuri wa mpira wa miguu. Wazo la kuelekea Chamwino likanijia, nilipanga kwenda kukutana na Mkude ili kujua nini ningeweza kupata kwake japo sikuwa na uhakika kuwa ningeweza kumkuta maana hata maelezo ya Dokta Gabriel yalikuwa na ukakasi ndanimwe.




Muda haukuwa rafiki kwangu na nilitakiwa kukimbizana nao kwa nguvu zote ilikuwa yapata saa nane na robo kwa mujibu wa saa yangu ya mkononi. Nilishapita Masika nikaicha ofisi ya Zima moto kisha Chuo cha ujenzi. Nilikuwa kimya sana huku ngoma za masikio yangu zikikumbana na sauti hafifu ya muungurumo wa injini ya gari langu nilifungua dashibodi na kutoa PK na kuimenya kisha nikaitupia kinywani mwangu ili angalau kuondoa harufu ya sigara. Nilikipita kiwanda cha Tumbaku TTPL kisha nikaifikia barabara kubwa iliyokuwa ikitokea kituo kikuu cha mabasi Msamvu wenyeji waliita Iringa road, nikaingia upande wa kushoto baada ya kuliruhusu gari kubwa la mizigo kunipita, niliongeza mwendo huku macho yangu kuliani yakikisoma kibao kilichokuwa kikiinadi nyumba ya kulala wageni ya Rhino na baa yake, mbele kidogo kushotoni nikilipita jengo kubwa la ibada la Jehovah's Witness Kingdom Hall, Jumba la Ufalme. Hapa nikapunguza mwendo wa gari yangu baada ya kuzipangua gia kisha mbele kidogo nikaingia upande wa kulia hapa nikapokelewa na barabara ya changarawe ambayo haikuwa na magari mengi sana hivyo kunipelekea kuwa huru kuongeza mwendo japo haukuwa mkali wa kuogofya, nilipishana na maduka mbalimbali ya vyakula, vibanda vya kuhudumu masuala ya pesa/ mawakala wa mitandao mbalimbali pia nilipishana na bodaboda nyingi sambamba na watembea kwa miguu ambao kwa kiasi fulani hawakuiacha barabara hiyo katika upweke. Dakika mbili mbele nilifika Chamwino mji ambao ulikuwa uko na majengo mengi ya hali ya chini, watu wake wakiwa ni wa maisha ya kawaida sana huku kukivuma sifa kede wa kede za vibaka waliyokuwa wakisumbua na kuwapa kero watu wa mtaa huo hasa nyakati za jua kuvaa koti. Niliipita mitaa hii na ile nikipita hapa na pale huku nikiyaridhisha macho yangu kwa mandhari halisi ya mtaa huu. Safari yangu ilikuja kukoma mara baada ya kuliona jengo moja lilioandikwa Nesige Mitishamba Clinic, nikajua nimefika mahala husika. Nikapoteza muda mwingi nikiwa hapo huku nikiyapa nafasi maelezo ya Dokta Gabrie Nyagile yabarizi kichwani mwangu, nikayasoma maelezo yote kwa utaratibu nilipojiridhisha nikaamua kuliacha gari langu taratibu kisha nikajisukuma nikiielekea nyumba moja ambayo ilikuwa ya hali ya chini sana paa lake likiwa limeezekwa kwa makuti na kukandikwa kwa udongo ambao nao ulianza kupapatuka na kuzifanya baadhi ya kuta kuwa na matundu mengi na mengine kuonekana yamezibwa na mapande makuukuu ya nguo/ mabwende. Hatua zangu zilinifikisha kwenye nyumba hiyo iliyoonekana kupoa kwa kiasi kikubwa sana, mlango wake ulikuwa wazi ukiwa umerudishiwa kwa kiasi fulani. Ilikuwa imejitenga sana nyumba hii mandhari yake ilikuwa chafu ambayo ilianza kuota nyasi sambamba na makusikusi mengine yaliyoashiria ufyekwaji wa nyasi hizo ilimradi yapunguze ghasia. Niliitazama nyumba hiyo kwa udadisi wa hali ya juu sana nikijaribu kuchungulia upande huu na ule ili kuweza kujihakikishia kama ningeweza kuona mtu ama chochote chenye kuweza kunisaidia. Nikajiridhisha kuwa hapa ndipo kwa Mkude kama maelezo ya Dokta Gabriel Nyangine yalivyo nadi. Sikuona kitu wala mtu hivyo ikanilazimu kuukabili mlango nikaugonga mara mbili kisha nikaweka utulivu nikisikiliza. Kimya kilikuwa kikuu, sikiridhika nikagonga tena mara mbili kisha nikatega sikio tena, nikasikia mchakacho ndani kuashiria kuwa kulikuwa na kiumbe ndanimwe.




"Nani anabisha hodi?...karibu?" Sauti kutokea ndani ikasikika, nilipoisikiliza vizuri ile sauti nikapata kujua mmiliki wa sauti hiyo hakuwa mwenye umri mdogo pia mmilikiwa wake akiwa ni mwanamke.




"Karibu mbona kimya?" Ilirudia hiyo sauti mara baada ya kuhisi ukimya ukiwa mwingi.




"Asante!" Nilijibu nikiwa na uhakika kwa sauti yangu angeweza labda kutoka kunisikiliza haikuwa hivyo.




"Ingia tu mama najisikia?" Iliniambia hiyo sauti ya mtu aliyeko ndani mh! Nikaguna huku nikiangaza macho yangu kila upande kabla ya kujiingiza ndani kwa utaratibu wa hali ya juu sana. Upande wa nje ulinasibu yaliyo kwa ndani ya nyumba hii, hakukuwa na vitu vingi vya kueleweka kulikuwa na mkeka ulionyambulika uliyoonesha kuwa ulikuwa ukitumika nje ya muda wake wa matumizi hata hivyo mkeka huo haukuwa wenyewe bali juu yake ulibeba mtu aliyekuwa amejifunika upande wa Khanga wenye bado kubwa la tundu katikati, mtu huyo alikuwa akitetemeka sana baridi.


Ilistaajabisha!




Baridi wakati hadi majira hayo jua lilikuwa bado likiwaka kwa hasira na sifa....? Huwenda kweli alikuwa mgonjwa. Nikazidi kuyatembeza macho yangu kila mahali, nikaona mabundu kadhaa yakiwa yamesimikwa kila mahala hapo sebuleni, kulikuwa na kochi moja la kizamani likiwa mbavu nje hakuna foronya wala chenye kunasibisha nayo, kuta za nyumba hiyo hapo sebuleni zilisilibwa kwa tope jekundu huku kwa mabatomabato rangi ya chokaa iliyochoka ikionekana kwa mfifio.




"Karibu....karibu kiti ukae dada!" Alinikaribisha yule mwanamke pale chini ambaye sauti yake ilikuwa ikilazimishwa kutokea kinywani dhahiri ya shahiri. Nikatazama kiti nilichotakiwa kukaa nikaona hakukuwa na kingine zaidi ya lile kochi lililovuliwa thamani yake na kuachwa uchi kidhalili. Sikuwa na hiyana nililisogelea nikalitazama kwa mtindo wa kulikagua kisha nikajiketisha.




"Karibu sana!" Akaniambia huku akijinyanyua kutokea pale mkekani na kuketi kitako mgongo wake ukipata msaa wa kupokewa na ukuta unaoumiza ukiegama hata hivyo alizoea.


Mazoea yanatabu!




Akanitazama akiwa na wasiwasi usoni mwake sura yake nilipoitazama nilimgundua kuwa alikuwa yupo kwenye hofu kubwa ya maradhi ya homa iliyomkumba lakini pia sura hiyo hiyo ilibeba ulizo la mtu aliyemtembelea maana sikuwa miongoni mwa wageni ambao aliwatarajia au aliwazoea.




"Nani mwenzangu?" Hatimaye akalifukuza jinamizi la kujiuliza moyoni bila mafanikio na kuamua kunitupia muhusika swali hilo.




"Bilashaka unaumwa dada yangu?" Badala ya kujibu alichoniuliza nikajikuta nikivutiwa na kumuuliza swali jingine huku lile la kwake nikilitia kwapani.




"Acha dada yangu Malaria imenibana vibaya sana ni siku ya pili sasa hata hivyo naona ni kama mwezi hadi najiuliza hii ni homa au nimesukumiwa jini lije kunimaliza....kwa lipi sijui mwana wa marehemu ni nisiye na ndururu macho nanga paa, damu ya mkopo mwili walegalega phu!" Alinijibu na kutoa shutuma za wasiwasi za kigonjwagonjwa halafu akajipumbaza mwenyewe na kuikashifu humohumo hali yake ya kimaisha.


Nilimhurumia.




"Sasa umejuaje kuwa unaumwa Malaria?" Nilimuuliza kwa udadisi maana asingeshindwa kuniambia kuwa amekwenda kupiga ramli.




"Nimetoka kupima muda si mrefu kutokea sasa hapa unionapo nimeandikiwa midawa hiyo! Hata sijui nainunua na bulungutu lipi maana hapa nilipo sina hata shilingi mia ya Tambiko," alinijibu huyo mama kiasi nikataka kuangua cheko kwa maneno yake lakini sikuona sababu ya kunifanya nicheke. Nilimtazama kwa kumhurumia kisha nikayazungusha macho yangu kuitazama ile sebule huku nikiwa na uhakika mkubwa kuwa macho ya mwenyeji wangu yalikuwa yakinitazama mimi.




"Usijali utapona," nilimwambia kisha pasipo kumpa nafasi ya kujibu nikamchomekea mada nyingine ambayo hasa ndiyo iliyonifikisha hapo.




"Samahani mama nilikuwa nina jambo ningependa uniruhusu nikuulize?" Nikamtazama kwa kina.




"Uliza tu dada, uliza!"




"Namuulizia mzee mmoja anaitwa Mkude nimeambiwa ni mzee maarufu na hii ndiyo nyumba yake?" Nikamuuliza hata hivyo nikamuona akishangaa kidogo kisha kunitazama kama vile ndiyo kwanza naingia nyumbani kwake.




"Aliyekuelekeza hapa ni nani?" Alinitupia swali baada ya kuvuta tafakuri.




"Kwani unamfahamu au hapa ni nyumbani kwake kweli?" Nikamuuliza nikilizunguuka swali lake na nilijua kwa asilimia kubwa ni lazima aingie mkenge kwani maswali kama hayo wanaoyashtukia ni watu weledi pekee wajuao namna ya kuling'amua swali na kulikwepa si huyu.




"Pengine Mkude unayemuulizia wewe siye nimjuaye mimi.....Mkude nimjuaye mimi kweli alikuwa akiishi hapa lakini ni muda sana na huu ni mji wake. Alifariki yapata miaka nane sasa tangu kufariki kwake hadi sasa wewe uniulizapo ni lazima nipandwe na taharuki na alama ulizo itande kichwani mwangu, Mkude ni baba yangu na mimi pekee ndiye mwanaye hakuwa na mtoto mwingine na ndiyo maana umenikuta hapa je, Mkude huyu ndiye uliyekuwa ukimuulizia au kuna mwingine?" Alieleza kwa kirefu kisha akaniuliza swali mwishoni nikabaki nimebung'aa kwa muda mfupi nikitafakari yangu. Niliyakumbuka maneno ya Dokta Gabriel Nyagile aliposema kuwa hadhani kama mtu huyo ni hai maana hata kipingi ameacha kumuona alikuwa tayari amezidiwa ujanja na umri hata hivyo ni muda umepita hakuweza kumtia kwenye mboni ya macho yake.




"Nini kilichokuwa kikimsibu mzee wako?" Nilimuuliza badala ya kumjibu, huwenda alishangaa mahojiano yangu naye hata hivyo hili halikunisimamisha wala kunipa hofu.




"Ni maradhi ya uzeeni umri ulimuacha mbali sana akadhoofu mwili na kukosa nguvu hata kifo kilipomchukua nilisema hewala! Maana uchago wa mkusanyiko wa matambara na kamba kitanda ulimkomba nyama za mwili ramani ya fito za mbavu zake zikajianika mwilini mwake kama Skeletoni ya Chura wa kale kwenye jumba la makumbusho." Aliongea mama huyo nikakosa namna ya kufanya.






"Ni maradhi ya uzeeni umri ulimuacha mbali sana akadhoofu mwili na kukosa nguvu hata kifo kilipomchukua nilisema hewala! Maana uchago wa mkusanyiko wa matambara na kamba kitanda ulimkomba nyama za mwili ramani ya fito za mbavu zake zikajianika mwilini mwake kama Skeletoni ya Chura wa kale kwenye jumba la makumbusho." Aliongea mama huyo nikakosa namna ya kufanya, kichwa kikaingia kwenye mawazo mengi sana nikatamani kuomba kuikagua nyumba hiyo kama ningeweza kupata chochote kuhusiana na usuhuba uliyopo baina ya Dokta Lumoso Papi Mmbai na Mzee Mkude lakini kila nikimtazama mwenyeji wa nyumba hii wazo langu nikalitupilia mbali kabisa kisha nikamuaga huku nikimpa noti mbili za shilingi Elfu kumi ili aweze kwenda kununua dawa apate kujitibia. Alinishukuru hadi nikahisi alitaka kumsahau Mungu aliyemuumba na nikajihakikishia kama nisingeondoka haraka huenda angenifananisha na malaika aliyewahi kumuota ndotoni ambaye alimtabiria furaha kwenye dunia ya dhiki na maisha yenye masimango.


Jangwa lilipata mvua ya mawe.


Nikarudi hadi lilipo gari langu nikafungua mlango na kujiingiza nyuma ya usukani kisha nikaamua kuondoka kwani nilikuwa na mizunguuko mingine binafsi nikishatoka kwa mwalimu Daniel Matia Okale.




____________




MWAMBIJE MKAMI ALIAMUA KUKICHEZESHA KITI CHAKE CHA OFISI VILE APENDAVYO aliamua kujizungusha kitini hapo kama Tufe. Kichwani mwake kulikuwa kumejaa mambo mengi sana kuhusiana na kazi hiyo ngumu ambayo alipewa na muheshimiwa Rais. Ilikuwa kazi ngumu sana yeye kuweza kuchukua kazi hiyo ya upelelezi kutoka mikononi mwa aliyekuwa kiongozi mkuu wa kikosi kazi hicho cha tume ya uchunguzi juu ya upotevu wa madaktari bingwa wa magonjwa sugu nchini aliyefahamika kwa jina Charles Kiango ambaye baada ya kustaafu maradhi yaliyomtesa kwa muda mrefu yakamletea kifo kilichomuweka mbali na ya walimwengu. Kazi hii ilimuumiza kichwa kutokana na kwamba ilisimama bila kujulikana kwanini ilisimama na tangu kusimama kwake tayari ilikatika miaka karibia tisa hivi na ushei, pili wahusika waliyopewa kazi hii hawakuwa na majibu yenye kuleta msaada wa kuweza kuendelea na hicho alichopewa. Alipoteza muda mwingi sana ofisini hapo bila kupata majibu yenye kumridhisha. Kitu pekee alichokuwa akikisubiri mahala hapo ni majibu kutoka kwa vijana alioweza kuwatuma kazi hiyo ya kuanza kupeleleza kuhusiana na namna madaktari hao walivyopotea. Alikuwa na imani na vijana wake watatu ambao aliwapa kazi hiyo ya kuhakikisha chanzo kikuu kinapatikana. Hakuvunjika moyo kwani kazi ilikuwa bado mbichi na vijana hao walikuwa na ari ya kufanya kazi akaamua kusitisha zoezi lile la kuzunguuka na kiti na kukilaza kichwa chake kwa nyuma akizikaribisha tafakuri kadhaa ziweze kumfariji.




Mara baada ya kupewa kazi hiyo Sembuyagi Mpauko Haufi sambamba na vijana wenzake wawili walijijaza katika usafiri wakitokea jijini Dar es salaam kuuvamia mji wa Morogoro. Walifika mjini hapo majira ya saa tatu na dakika zake hivyo hawakujipa muda wa kupumzika kwa hata sekunde ndogo walichokifanya ni kuelekea moja kwa moja Msamvu nyuma ya Makuti Bar ambapo Daktari Omary Maboli Siki alikuwa akiishi. Hii ilikuwa ni kabla ya Catherine kufika eneo hilo. Waliiacha gari yao kwa umbali wa kutazamika kisha wakachepuka na chochoro iliyokuwa ikiwafikisha kwenye nyumba aliyokuwa akiishi Daktari huyo. Ukimya wa pale ulitosha kuwawezesha kufanya yao kwa nafasi kubwa bila kuwa na hofu ndani yake. Waliuvamia mlango kwa funguo zao na kuingia ndani ambako walilakiwa na vumbi kali lililowafanya wapige chafya mfululizo. Walifunua hapa na pale wakachangua hiki na kile bila kuwa na utaratibu elewevu ndani mule kukawa shaghalabaghala hovyohovyo na wasiambue kitu chochote cha maana zaidi ya picha kadhaa za 'Black and White' za kizamani, zilizojazana kwenye albamu ndogo ambayo ilikuwa imewekwa ndani ya kichanja cha meza iliyopo sebuleni. Walichanganyikiwa kwa asilimia kubwa sana. Sembuyagi yeye si kama alikuwa mgeni kwenye kesi hii la! Bali alichotaka kukifanya ni kuhakikisha upekuzi mzito zaidi ambao haukufanyika awali kipindi alipokuwa na jopo jingine la wanausalama angali akiwa kijana mwenye nguvu zaidi ya hapo ambapo umri ulikuwa ukimuacha taratibu, unafanyika kikamilifu bila kuacha mambo ya muhimu ambayo yangeweza kuwasaidia kwenye kazi hiyo. Walipoteza muda mwingi na wasipate kitu wakatepeta nguvu miilini mwao.




"Hakuna kitu kabisa hapa?" Aliongea Mabule akiwa anatokea kwenye chumba cha kulala.



ITAENDELEA


     


Simulizi : Mpango Wa Nje - Ni Pigo Butu La Kifo 


Sehemu Ya Pili (2)




"Umetafuta kila mahali?" Aliuliza Sembuyagi.




"Kila pembe ya chumba sijaona kitu,"




"Hata mimi kwa upande wangu ni hivyohivyo zaidi nilichopata ni kitabu cha kutunzia kumbukumbu ambacho ndani kimebeba namba za simu na si nyingi sana ni kama tatu hivi na zinaonekana ni simu za ofisi!" Aliongea Jackson akielezea kwa upande wake huku akimkabidhi kile kitabu Sembuyagi. Sembuyagi alikitazama kwa mlolongo wa sekunde fupi kisha akawatazama usoni wenzake.




"Ni shirika gani la mawasiliano hili....? Hata hivyo haina haja ya kujadili sana tutajua tu." Akasema Sembuyagi kisha wakatoka na kuufunga mlango kama walivyoukuta wakalielekea gari lao safari ya kuelekea nyumbani kwa Dokta Lumoso Papi Mmbai ikaanza. Ukimya ukiwa mkubwa garini wakafika maeneo ya Tanesco hapa bila kujua wakapishana na gari ndogo nyeupe, hiyo gari haikuwa nyingine bali ni Toyota Corola iliyokuwa ikimilikiwa na Catherine. Walifika Soko la Kikundi ikiwa inakita saa saba na dakika arobaini na tano usiku huku mvua kubwa bado ikiwa inaendelea kuchapa. Wakatumia njia ileile kuingia ndani nako wakakaribishwa na muonekano uleule wa vumbi na utulivu mkubwa. Kurunzi zao zikiwa imara kabisa kuhakikisha wanaona kwa uhakika. Nyumba hii ilikuwa tofauti na iliwafanya wagande mlangoni kwa muda kidogo mara baada ya kuingia kabla ya kuamua kuendelea na safari yao ya kuikagua. Kulionekana alama ya soli ya kiatu, walipoitazama alama hiyo kwa uzuri wakagundua kuwa ilikuwa ni ya kiatu chenye soli ngumu lakini isiyoleta kelele wakati wa mjongeo. Waliona mchanga mbichi kuashiria kuwa mtu aliyeingia ndani humo hakuingia muda mrefu sana na aliingia wakati mvua inaendelea kunyesha au ilikuwa inaanza kunyesha. Wakapiga hatua zao taratibu huku silaha zao zikiwa mikononi tayari kwa kufanya shambulio lolote litakaloibuka. Walishangazwa na hali ya nyumba ilivyo ni kama haikuwa imepekuliwa.




"Inamaana huyu mtu aliyeingia humu ndani hakufanya jambo lolote?" Akauliza Mabule akiwa anaitazama meza sebuleni ambayo ilihanikizwa na vumbi na seti moja ya makochi ya toleo la zamani. Meza hii walipoitazama kwa umakini sasa wakagundua ilikuwa imekaliwa na kitu juu yake. Lile wazo la kuwa haikukaguliwa wakalifuta akilini mwao.




"Mh!" Akagumia kwa ndani Sembuyagi kabla ya kuzungumza.




"....Tumetanguliwa na mtu wa kazi humu ndani....?"




"Kwanini uamini hivyo kuwa aliyeingia humu ni mtu wa kazi?" Akauliza Jackson akiwa anaumulika mwanga wa Kurunzi yake kwenye rafu ya vitabu na mafaili mbalimbali sebuleni hapo.




"Hakuja tu ilimradi kaja, kuna kitu amekifuata humu ndani na ni mpelelezi makini sana. Ukiangalia kwa umakini utagundua hii nyumba imekaguliwa tazama mezani kuna alama ndogo sana ya mguso kama si wa kidole basi ukucha na inaonekana kulikaliwa na kitu ambacho alikuwa akikikagua maana hata vumbi limetavangwa, angalieni na mwenendo wa hatua zake kutokea kwenye kila chumba inaonekana chumbani hakwenda kabisa, jikoni mara moja akarudi lakini kwenye chumba cha uchunguzi alikwenda zaidi ya mara moja na kurejea hapa sebuleni na angalieni alifika hadi hapa kwenye kiunganishi cha umeme na mkizidi kuangalia mtagundua kuwa kuna kazi ilifanyika hapa si bure." Alitoa maelezo yake Sembuyagi akiwa kwenye umakini wa hali ya juu sana akiutazama mwenendo wa mtu aliyewawahi kama wanavyohisi.




"Ingieni kula mahali muangalie kwa umakini sana na muhakikishe hamchangui kitu chochote kwani sasa nauona ugumu wa hii kazi huwenda kazi hii inamdudu ndani na sijui yupo kwa misingi ipi, mdudu huyu anaonekana anatumia akili nyingi kuliko hata uwezo wa akili ya binadamu wa kawaida. Sina imani kama tunaweza kuambulia kitu humu ndani lakini hatuwezi kuacha kuchakua kuweni makini nimegundua tunafanya kazi kitoto sana wakati kuna mtu au watu wanajua wakifanyacho." Alisema huku akiwa anayazungusha macho yake kila upande. Aliganda pale sebuleni mithili ya mtu achezeshwae mchezo wa kitoto wa 'Kinongo'.


Aliganda.




Vijana walirudi tokea kila upande wa chumba na wasiambulie kitu kabisa hili liliwatanabaisha kuwa sasa wako kwenye kazi ngumu. Hawakupoteza muda waliondoka kisha wakaelekea kwenye hoteli ya Mt. Uluguru ambako ndiko walikofanya Booking ya malazi. Usiku huo huo bila kusubiri asubuhi, simu ilipigwa kwa mkuu wao kutoka usalama wa taifa idara ya upelelezi aliye juu ya kazi hiyo aliyowapatia kuelezwa kila kitu kilichotokea. Hamaniko lililomkumba Mwambije Mkami usiku huo lilikuwa ni la aina yake na kama angelikuwa ameoa basi hata mkewe angelimpaishia usingizi wake. Alichanganyikiwa na kujikuta akikosa utulivu. Kila kitu kilifanywa siri na siri hiyo yeye hakuambiwa sasa kwanini asipagawe pale alipopewa taarifa hiyo ya kuwepo kwa mpelelezi mwingine au mtu yeyote mwenye dhamira kama yao.




"Unataka kuniambia kuna mtu anapita mlimopita?" Akauliza kwa kihoro Mwambije Mkami.




"Sisi ndiyo tumepita alipopita mkuu!" Jibu la kuogopesha likamkuta Mwambije Mkami akiwa ameachama kinywa chake kama Sawaka mwenye njaa mbele ya kitoweo cha Mbwa aliyemvunjavunja mifupa yake, akajikuta anapata mwayo wa mhadaiko usiokuwa na mantiki yoyote akanyanyuka kutokea kitandani akasimama katikati ya chumba chake kama anayekihubiria kitanda.




"Sembuyagi, unataka kuniambia hakuna mlichoambua hata kimoja kwenye uchunguzi wenu?" Akaongea Mwambije.




"Hapana, hatukukosa kabisa, nyumba ya Daktari Omary Maboli sisi tuliwahi hivyo tukafanikiwa kupata kitu kimoja tu ambacho angalau kinaweza kuleta mwanga."




"Nini?"




"Kitabu cha kuhifadhia kumbukumbu na ndani yake kuna namba tatu za simu."




"Hivyo tu?"




"Hakuna ziada mkuu?"




"Mnauhakika sasa kuwa mnaweza kuambua kitu humo kupitia hizo namba....? Msilete mchezo wa kuigiza Sembuyagi hili tukio ni la muda mrefu hata hivyo sina hakika kama namba hizo zinaweza kuwa zinapumua." Aliongea Mwambije akiwa haelewi mwanzo wala mwisho ni kama aliyekuwa akining'inia katikati halafu maandalizi ya kukokwa kwa moto yakiandaliwa kwa sifa bila jasho huku wakokaji wakijilamba ndimi zao kwa kumtamani angali mbichi, alijifananisha na ndafu. Akatoa agizo kali kwa vijana hao kuwa wahakikishe wanazifanyia upekuzi wa kina hizo namba na wajue mahali ambapo wangeweza kuanza.




_______




Asubuhi kulipopambazuka kuliibuka mshikemshike wa nguvu kwa vijana hao watatu maana ilikuwa ni lazima wajue bara na pwani. Hatua ya kwanza waliyoamka nayo ilikuwa ni kuvamia kwenye jengo linalomilikiwa na mtandao mmoja wa mawasiliano ya simu na aliyefanya kazi hiyo alikuwa ni Mabule. Aliingia ndani ya ofisi moja ya maulizo akajifikiria kama angeweza kupata huduma stahiki, utazamaji wake haukuwa wa kujizubaisha hata kidogo ingawa ilikuwa ni mara yake ya kwanza kufika kwenye jengo hilo, aliyazungusha macho yake kwenda kulia na kushoto hadi alipomuona kijana mmoja aliyekuwa ameinamia tarakilishi akicharaza kitu kupitia kicharazio cha tarakikishi hiyo. Akapiga hatua kumkabili kisha akajiketisha kwenye kiti kilichopo mbele ya kijana huyo.




"Habari za Asubuhi?" Akauenzi uafrika Mabule akiliacha tabasamu lilingane na salamu yake.




"Salama karibu?" Alijibu huyo kijana huku akijaribu kuufukuza mshtuko uliompata mara baada ya ugeni wa ghafula kuwa mbele yake.




Aliingia ndani ya ofisi moja ya maulizo akajifikiria kama angeweza kupata huduma stahiki, utazamaji wake haukuwa wa kujizubaisha hata kidogo ingawa ilikuwa ni mara yake ya kwanza kufika kwenye jengo hilo, aliyazungusha macho yake kwenda kulia na kushoto hadi alipomuona kijana mmoja aliyekuwa ameinamia tarakilishi akicharaza kitu kupitia kicharazio cha tarakikishi hiyo. Akapiga hatua kumkabili kisha akajiketisha kwenye kiti kilichopo mbele ya kijana huyo.




"Habari za Asubuhi?" Akauenzi uafrika Mabule akiliacha tabasamu lilingane na salamu yake.




"Salama karibu?" Alijibu huyo kijana huku akijaribu kuufukuza mshtuko uliompata mara baada ya ugeni wa ghafula kuwa mbele yake.




"Asante sana pole na majukumu?....niko na shida tafadhali?" Akarudisha jibu na kutumbukiza ombi kwa muambatano.




"Naweza kukusaidia?" Akauliza yule kijana akiwa anatabasamu kama ada ya ukarimu kwa mteja. Mabule akatoa kile kitabu kidogo kutokea ndani ya mfuko wake wa koti la suti kwa upande wa ndani chini kidogo ya kwapa akakitua mezani baada ya kukifungua kwenye kurasa husika kisha akakisogeza kwa vidole viwili vinavyokaribiana macho yake akiyabung'aza usoni mwa kijana huyo akizidi kuchanua tabadamu la kirafiki. Kijana yule akaipitishia macho ile karatasi kishapo akamtazama mteja wake usoni.




"Msaada gani unaotaka nikupe?" Aliuliza huku akiivuta tarakilishi yake na kuhitaji kuendelea na kile alichokuwa akikifanya mara baada ya kumtoa kwenye umuhimu mteja wake mara baada ya kutazama zile namba kitabuni na kumuona mteja huyo hakuwa na tija kwake.




"Nahitaji kujua kama hizi namba bado zinatumika au kama hazitumiki, zilikuwa zikimilikiwa na nani na mahali ambapo zilikuwa zikitumika?" Akauliza Mabule huku akilitoa tabasamu usoni mwake na kuweka umakini. Tabasamu la dhihaka likamtoka yule kijana kisha akaanza kubofya vitufe kadhaa kwenye tarakilishi yake akimpuuza mteja huyo.




"Hakuna kitu kama hicho na huwa hatudili na huduma za namna hiy....!" Alikuwa hajafika tamati, kitambulisho cha kazi kikamtoka Mabule na kukitua mezani. Yule kijana akakikata jicho katika namna ya kukisoma kisha kumtazama kijana huyo usoni akiwa kama anayehakiki mshabaha wa picha iliyobebwa na kitambulisho kile na mbeba kitambulisho. Kisha akakivuta kile kitabu na kukitazama upya kwa utaratibu.




"Ni kazi ngumu sana kwanza mtandao huu kuna wakati ulizorota katika ufanyaji kazi sasa sina hakika kama tunaweza kufanikisha hili kwa uhakika hata hivyo ni nje ya utaratibu wa kazi yangu." Akasema yule kijana.




"Najua na ndiyo maana nikaja moja kwa moja hapa sikutaka kupitia kona nyingi." Akajibu Mabule akiwa na uhakika wa kazi yake kufanyika. Alikirudisha kitambulisho chake kwenye mfuko wa shati na kulirudisha tabasamu la matumaini.




"Kuwa na subira kidogo kwa dakika kadhaa," akasihi yule kijana kisha akanyanyuka na kumuacha mteja wake akipata wasaa wa kuuacha mwili na akili yake utazame vya ndani akanza kuhisi kuwa kulikuwa na kiyoyozi kilichokuwa kikitekeleza majukumu yake ipasavyo ilhali hapo awali hakuwa amehisi hilo. Akajaribu kuyazungusha macho yake hapa na pale katika namna ya kuyapa chakula kisha akajituliza tena akili yake akiirudisha kitini akijitazama kuanzia mapajani hadi tumboni pasipo na sababu za msingi za kufanya hivyo mwishowe akayahamishia macho yake mezani na kuishangaa tarakilishi kwa namna ilivyompa mgongo.


Ni katika namna ya kusubiri tu.




"Nimechelewa kidogo kaka, unajua bwana haya mambo yanahitaji muda na utulivu sasa inapokuwa haraka hivi kuna baadhi ya kazi inabidi zisimame kwa sekunde kadhaa na kufanya hivyo ni kumvuta ndevu bosi," aliongea huyo kijana akijikalisha kitini mwake kisha akaivuta tarakilishi na kuitazama kwa muda kisha akaingiza vitu fulani alivyokuwa akivinakili hadi alipomaliza akapoteza muda wa sekunde nyingine nyingi kama siyo dakika kisha akaigamia kitini.




"Utanisamehe sana kwa kukutoa nje ya majukumu yako kama unavyojua shughuli zetu zinavyotegemeana." Akaongea Mabule katika hali ya kuomba radhi.




"Usijali, kazi imekamilika. Ilikuwa ikienda kuwa ngumu lakini nikajua iko namna ya kufanya jitihada, namba mbili hazijaleta majibu ya aina yoyote ile isipokuwa moja," akaweka koma na kuchukua kalamu na kuiandika namba hiyo kwenye kile kile kijitabu cha kumbukumbu kilicho na jalada gumu lenye rangi ya buluu iliyoiva.




"Hii ndiyo inayotumika hadi sasa japo inaonekana ilianza kutumika kwa miaka mingi iliyopita karibia miongo miwili sasa. Ni namba ya ofisi hii na tumegundua maongezi ya mwisho yaliyofanyika kupitia namba hii. Ningekusikilizisha kama kungekuwa na uwezekano huo hata hivyo hayana mantiki sana lakini msaada wa kuweza kukusaidia ni huu hapa; Nenda Hospitali ya mkoa muulizie mtu anayefahamika kwa jila la Dokta Gabrile Nyagile. Huyu anaweza kukusaidia kujibu maswali yako na imekuwa rahisi kwa kuwa ndiye pekee aliyetajwa kwenye mazungumzo niliyoyanasa....ni hatari sana kufanya hivi na natoka nje ya maadili ya kazi yangu tafadhali nenda." Alimaliza kutoa maelekezo yule kijana huku akiwa na wasiwasi sana na kama isingelikuwa Mabule kutoa kitambulisho kilichomtambulisha kama mkaguzi wa polisi, huwenda asingekuwa radhi kuifanya kazi hiyo. Mabule akashukuru na kukichukua kile kitabu kutokea mikononi mwa yule kijana huku akimbabatiza na noti mbili za shilingi elfu kumi.




"Asante sana kwa msaada wako nadhani nikiwa na shida zaidi nitakuona," akashukuru kiungwana Mabule huku akiondoka eneo hilo taratibu.




"Ah..a aaaa!" Yule kijana akabaki akichachawa akitaka kusema neno hata hivyo akajikuta mikono akiining'iniza hewani huku atakaye kusema naye akiondoka kwa mwendo wa haraka akiwa tayari ameukaribia mlango. Akajikuta akigeuza macho yake huku na huko akitazama watu kisha akajikalisha kitini akiwa na uhakika wa mlo mzuri wa mchana.




___________




Hata walivyomaliza harakati zao wakajikuta wameumumunya muda mwingi sana, si kama hawakujua kuwa mbele yao walitakiwa kwenda kumuona Daktari Gabriel kwa ajili ya mahojiano naye ya kina la! Ila kuna wingi wa mambo uliwapotezea wakati hata walivyomaliza shughuli hizo ilikuwa tayari ni saa nane na dakika nyingi tayari. Walifika kwenye Hospitali hiyo ya mkoa huku wakiwa hawana uhakika kama mlengwa wangeweza kumkuta. Wakaamua kumuulizi Daktari Gabriel kwa kubahatisha, wakaelekezwa mahali ofisi yake ilipo wakaelekea huko. Walivaa suti nyeusi na mmoja wao akiwa amevaa miwani ya giza na aliyevaa hivyo alikuwa ni Sembuyagi Mpauko Haufi. Waligonga mlango baada ya kuukaribia wakakaribishwa na mwenyeji wa ofisi hiyo ambaye ndiyo kwanza alitoka kuagana na Catherine na kwa majira hayo akiwa anajiandaa kutoka kabisa hospitalini hapo kwani muda wake wa kuwajibika kwa siku hiyo ulishakatika na hakuona haja ya kwenda kula kisha arudi.


Bahati ilikuwa upande wao.




Dokta Gabriel Nyagile alipatwa na mshangao kiasi kwa kupokea mlolongo wa wageni wasiyokuwa rafiki kwenye utaratibu wake wa kazi.




"Karibuni mkae!" Akawakarimu wageni hao ambao ni kama viti vya kukaa hawakuviona walikuwa wakiitazama ile ofisi kwa marefu na mapana yake.




"Asante sana Dokta habari za kazi?" Akajibu ukarimu ule Jackson akiwa amesimama karibu na rafu ya vitabu.




"Kazi inakwenda vizuri karibuni sana niwasikilize shida zenu tafadhali," aliongea Dokta Gabriel akiwatazama akiwa amesimama wima asiyejua akae au aendelee kusimama vivo hivyo.




"Sisi ni maafisa usalama kutoka usalama wa taifa kitengo cha upelelezi nafikiri tuko na Dokta Gabriel Nyagile?" Akajitambulisha Sembuyagi Mpauko kwa niaba ya wenzake. Dokta Gabriel aliwatazama kwa tuo huku kichwani mwake akiilaani siku hiyo kwa kuwa haikuwa siku njema kwake.




"Ndiyo, ni mimi karibuni?" Akawakaribisha kuku akimuonesha kiti Sembuyagi ambaye hakuwa na muda wa kukaa na badala yake akaikita mikono yake mezani na kumtazama Dokta Gabriel usoni akisema.




"Tuko hapa kwa shida moja ambayo itaambatana na maswali machache kama utakuwa radhi kutukopesha ushirikiano wako." Akaweka tuo na kumtazama Daktari huyo kwa macho yasiyotulia kisha akamalizia.




"....Natumai unawafahamu watu wawili muhimu sana ambao walikuwa wakifanya kazi pamoja nawe hapa Hospitali, Dokta Lumoso Papi Mmbai na Dokta Omary Maboli Siki...?" Akaweka ulizo kisha akamkazia macho usoni. Dokta Gabriel akatafuta utulivu kwa kujiweka kitini kwake kisha akavuta pakiti la sigara na kuchomoa sigara moja akaitupia kwenye kingo zake za midomo akasogeza kiberiti cha gesi akaiwasha. Akatoa moshi mchache kwenye pembe za midomo yake huku akimfikiria binti ambaye aliagana naye punde hasa kilichopelekea amfikirie ni onyo la kutokusema chochote kwa mtu yeyote kuhusiana na ujio wake mahala hapo.




"Hawa watu nawafahamu?" Akajibu kwa utulivu huku akipachika tena sigara kwenye kingo zake za mdomo.




"Unawafahamu kwa namna gani licha ya kuwa walikuwa ni madaktari wenzio na mliokuwa mkishirikiana katika utendaji kazi?" Akauliza Mabule akiwa anajisogeza karibu na ile meza. Dokta Gabriel akavunja shingo lake na kumtazama kijana huyo kwa makini kisha akauliza.




"Kwanini mnauliza maswali haya magumu namna hii?"




"Kama tulivyo sema awali kuwa sisi ni maafisa usalama (akaonesha kitambulisho cha kazi). Tunapeleleza upotevu wa madaktari wenzako ambao walipotea kwenye mazingira tatanishi hivyo taifa kama taifa lililo na serikali imara haliwezi kuvumilia upoteaji wa watu wake hata kama ni wenda wazimu kiasi gani kisha kukaa kimya pasipo na jitihada zozote za kuzuia." Akajibu Sembuyagi.




"Ni muda mrefu umepita hadi ile hofu ya kuwa baada ya wale huwenda nikawa mimi na wengineo imefutika, unadhani kwa kipindi cha miongo miwili yote kuna lolote linaweza kusaidia hawa watu wapatikane?" Akauliza Dokta Gabriel Nyagile akiwa kwenye utulivu huku njaa aliyokuwa akiisikia akiipa usugu wa kuidumaza kwa moshi mwingi wa sigara avutayo.




"Hata kama wamekufa lakini mifupa yao ipatikane kupitia hilo tutakuwa tumejua pa kuanzia?" Akajibu kwa ukali Jackson akiwa anamtazama Daktari huyo usoni. Dokta Gabriel Nyagile akamtazama kijana huyo kwa kitambo kifupi kisha akatikisa kichwa kwa masikitiko makubwa ya kufokewa na mtoto wa kuweza kumzaa ilhali hajui sababu ya kufokewa kwake.




Madakta walipotea kwa kutekwa...kama ni hivyo kweli yeye anahusika na nini hadi akalipiwe na kijana yule mdogo. Huo ulikuwa ni ukosefu wa adabu. Akahisi uchungu mkubwa sana moyoni mwake akajilaumu kwanini hakuwa na hamu ya kuhitaji mwanamke tangu awali huwenda leo angekuwa na kijana mkubwa kumzidi huyo afisa usalama anayemkalipia kama tu angejihusisha na wanawake. Mwisho akailaumu kazi ya udaktari ambayo ilimuweka katika muda mwingi akisoma na kutafiti hadi kuchelewa kujihusisha na wanawake hata hivyo moyoni alifarijika baada ya kuikumbuka sigara, moyo wake ukatabasamu na tabasamu lilipozidi uzito, moyo huo wa nyama laini kama pamba ya daraja la kwanza, ukaangua cheko la matumaini huku ukimzihaki huyo kijana kuwa hata kama hana mtoto mkubwa kama yeye hata hivyo alikuwa na zaidi ya mke ambaye ni sigara. Huyo pekee alikuwa ndiye ubani wa moyo wake.




"Kwa maana hiyo mnadhani mimi najua ni wapi rafiki zangu Dokta Lumoso Papi Mmbai na Dokta Omary Maboli Siki walipo?" Akauliza kwa unyonge mkubwa sana.








moyo wake ukatabasamu na tabasamu lilipozidi uzito, moyo huo wa nyama laini kama pamba ya daraja la kwanza, ukaangua cheko la matumaini huku ukimzihaki huyo kijana kuwa hata kama hana mtoto mkubwa kama yeye hata hivyo alikuwa na zaidi ya mke ambaye ni sigara. Huyo pekee alikuwa ndiye ubani wa moyo wake.




"Kwa maana hiyo mnadhani mimi najua ni wapi rafiki zangu Dokta Lumoso Papi Mmbai na Dokta Omary Maboli Siki walipo?" Akauliza kwa unyonge mkubwa sana. Sembuyagi akaelewa unyonge wa Daktari huyo bingwa wa magonjwa ya moyo na upasuaji akajishusha.




"Si hivyo mzee wangu, tunataka kujua chochote kile ambacho wewe unajua au ambacho walipata kukuambia kitu kuhusiana na dalili za kupotezwa au hata kupotea kwao." Alipoongea hivyo Daktari huyo akamtazama kwa muda kidogo kisha akasema.




"Kwenye kazi hizi mnafaa kuwapo watu wazima kama ninyi lakini si mabarobaro kama hawa. Labda niwaambie ninachokikumbuka kutoka kwa Omary Maboli Siki. Huyu bwana aliwahi kunigusia kuhusu vitisho alivyokuwa akivipokea, alisema yalikuwa ni kama maongezi ya kawaida hata hivyo kwa kadiri siku zilivyokuwa zikisogea maongezi hayo akayatafsiri kama vitisho maana yalikuwa yakimshinikiza kufanya jambo fulani...!"




"Yalikuwa ni maongezi gani hayo ambayo yaligeuka kuwa vitisho?" Alidakia Mabule na kuifanya kauli ya Dokta Gabriel kuning'inia hewani.




"Mh! Limekuwa fumbo kubwa hadi leo maana hakuwahi kusema ni nini anachoshinikizwa na hao wampao vitisho, kitu cha mwisho kuona kwao ni uchakalikaji wa mambo yao binafsi, sikutia shaka kwa kuwa walikuwa wakifanya kazi kubwa kwa taifa hili hata kuwa na maabara zao nyumbani kwa ajili ya kurahisisha utendaji hata hivyo nilikuja kugundua walikuwa wakitoka hadi nje ya mkoa huu mwisho wa yote ni kutokuonekana kwao kabisa." Akakoma hapo na kuivuta sigara yake taratibu huku akiwafikiria wapelelezi walivyo watu wa ajabu hakujua kwanini hawaaminiani hata kidogo wapewapo kazi hata hivyo alijipongeza kwa kuweza kuwazunguusha na wasimuulize chochote kama kuliwahi kufika mtu jamii yao.




"Unaamini walitekwa?" Sembuyagi aliuliza na Dokta Gabriel akamtazama mithili ya mtu atazamaye sanamu la utupu. Lilikuwa ni swali la kipumbavu sana aliliona.




Inamaana watu wazima kama wale wanaweza kuwa wamejipoteza ama kupotea pasipo sababu za msingi...? Kama ni ajali kwa nchi gani basi Tanzania wasijulikane ama kuonekana....? Akawaza akitikisa kichwa kukubali kuwa anao uhakika kuwa madaktari hao wametekwa. Hakujua nia na dhamira ya swali hili kutoka kwa mtu makini na mkongwe kwenye anga hii ya upelelezi. Alikuwa akitavangia miaka Ishirini na tatu sasa akiwa ndani ya kitengo hicho.




"Unadhani wametekwa...? Na nani...? Na watakuwa wametekwa kwa misingi ipi...? Mirengo ya kisiasa, kiimani ama ugomvi na chuki binafsi za mtaani...?" Akauliza tena Sembuyagi Mpauko akiwa makini na macho ya Dokta Gabriel. Dokta Gabriel akaomba utulivu kutoka moyoni japo kwa muda maana aliona jinsi anavyoingizwa kwenye mtego kwa akili nyingi.




"Taaluma yangu ni utabibu hivyo kujua sababu ya utekwaji wao nitaongopa." Akajibu Dokta Gabriel Nyagile akizidi kuimumunya sigara yake taratibu kama pipi ya kijiti watoto wanaita 'bigi bomu'.




"Kuna mtu yeyote alifika kabla yetu hapa kwako?" Hili lilikuwa ni swali la kushtukiza sana kutoka kwa Jackson kwa kiasi fulani lilimshtua Dokta Gabriel kwani hakuwa amelitarajia kama lingemjia kwa haraka kiasi hicho.




"Hakuna?" Hata hivyo alijibu kwa kujiamini kisha akaipachika sigara yake kinywani na kuivuta. Sembuyagi akanyanyuka kutokea pale kitini alipokuwa amekaa baada ya kunogewa na mahojiano yale kisha akamtazama Daktari huyo kifedhuli akapiga hatua moja nyuma baada ya kukisogeza kiti kushoto.




"Tunakwenda nadhani tunaweza kurudi muda wowote kujiridhisha na majibu yako." Akasema Sembuyagi kisha wakapiga hatua hadi kwenye mlango wa kutokea ofisini humo huku jicho la Dokta Gabriel likiwatazama. Vijana walio pamoja na Sembuyagi walitangulia kutoka lakini Sembuyagi alipofika kizingitini mguu ukagoma kutoka nje ya ile ofisi akaurudisha ndani na kugeuka akirudi huku hali ile ikiwasimamisha wale wawili.




"Umegoma kutusaidia kwa ushirikiano wa hiyari nadhani tunazo njia nyingi za kukuhoji nami sikutaka tuzitumie maana si salama kwa afya ya mwanadamu. Nikiitazama hii ofisi namuona mtu...namuona mtu ndiyo, namuona mtu ambaye alikuja hapa kwako na kukaa kwenye kiti nilichokaa mimi, mtu huyu alikuwa na maswali kama yangu na yaliyohitaji msaada kwako kama mimi nilivyouhitaji. Tofauti yangu na huyu mtu ninayemuona ni kwamba ulimjibu sawia na kirafiki kabisa huku mkishea pakiti moja ya sigara na kukung'uta majivu kwenye kikombe kimoja huku mimi ukinidanganya na kunizunguuka. Hisia zangu zinaniambia hivyo na huwa sipingani nazo na ndiyo maana ukaniona nimesita kutoka pale kizingitini." Akaweka tuo Sembuyagi huku akizidi kupiga hatua ya hapa na pale ofisini mule kwa tambo kubwa. Mshtuko ukamvaa Dokta Gabriel Nyagile baada ya historia ile ya kubuni ikiendana na ukweli ikitambwa na bwana huyo. Hakujua kuwa mshtuko ule ulikuwa ukienda kumpa majibu Sembuyagi kuwa kweli kulikuwa na kitu alikuwa akikificha kichwani mwake.




"Naweza kutumia njia yoyote mbaya kuanzia sasa kama hutaki tuwe marafiki kupitia mahojiano haya. Unataka kuniambia kuwa kweli humu ndani hakujafika mtu kabla yetu?"




"Hakuna ndugu yangu kama angelikuwapo mbona ningali kwambia, ukiona kimya ujue hakuna mtu aliyefika wa aina yenu!" Akajibu kwa kujiamini kiasi maana imani juu ya watu hao ilishapotea kabisa. Na hakutaka kwenda kinyume na makubaliano na yule binti ambaye alinadi kuwa alitumwa na suhuba wake wa zamani ingawa hakuwa akimuamini moja kwa moja.




Egama kwa kile unachohisi kuwa kina nguvu. Huu ndiyo usemi aliyoutumia Dokta Gabriel Nyagile.




Afanye nini akajiuliza hata hivyo jibu likachelewa.




"Ni nani alikuja kabla yetu na mkazungumza chochote kuhusiana na hili tulilokuuliza au hata tusilokuuliza?" Akauliza kwa sauti ya chini na nzito ambayo aliiulizia karibu zaidi na sura ya Dokta huyo baada ya kuikabili ile meza ya kiofisi.




"Sema ili usiumie.....!" Akaendelea.




"....Sema kabla sijaamua kubadilisha zoezi na namna ya kuhitimisha mahojiano haya au uko radhi tusafiri na wewe ukahojiwe mahali usipopajua?"




"Hapana siko taya....!"




"Basi sema unachojua kuhusiana na yule aliyefika hapa?" Akakazia Sembuyagi akiwa na uhakika ushindi utakuwa upande wake kwani dalili zote za kuwa mtu huyo anajua vingi zilijionesha. Dokta Gabriel Nyagile alikiinamisha kichwa chake kidogo chini akiwa kwenye tafakari pana mno alipokuja kunyanyuka akawa tayari amepata jibu la kuwapa.




"Kauli ya mwisho ya Dokta Omary Maboli Siki kabla ya kupotea ni siku nilipoongea naye simuni akaniacha na hii mara baada ya maongezi machachache ya hapa na pale. Alimtaja mtu anayeitwa Musa."




"Musa!" Akashtuka Sembuyagi kisha akamkodolea mimacho Daktari huyo hili jina Musa analikumbuka aliwahi kulisikia mahali ila akili yake ilikataa kumkumbusha ni wapi. Jicho hilo alimtazama kwa muda mrefu sana Dokta huyo kisha akainua mwili na kichwa chake akitafakari jambo hatimaye akawageukia wenzake hata hivyo sauti yenye hofu ikasikika ikisema.




"Kinyume na hilo jina Musa sina tena ninachokikumbuka hata kama mtanikata kichwa na kuuweka moyo wangu miguu juu kichwa chini, hakuna ninacho kijua." Wakamtazama hasa Sembuyagi alimtazama kwa kitambo kirefu ni kama aliyekuwa akikichambua kichwa cha Dokta Gabriel kisha kujiridhisha kuwa hakuna kitu kingine zaidi ya hicho.




"Kesi hii inabidi tuiwasilishe kwa mkuu kesho hili jina Musa niliwahi kulisikia mahali hivyo hakuna sababu ya kuweza kumbana huyu Daktari mzee wacha amalize ujana wake wa machweo salama salmini. Mkuu atatupa namna nyingine ya kufanya kupitia hili jina. Wakaondoka na kurudi kwenye Hoteli waliyofikia kwa lengo la kuupitisha usiku hapo ambao ulishaanza kubisha hodi ili ifikiapo siku nyingine warudi jijini Dar es salaam.




_________


Usiku ulikuwa umeshaichukua nafasi yake na kuvimbisha kifua na kuifanya nchi kuwa katika giza kila kona. Usiku huu ulikuwa hauna kelele nyingi sana sijui kwa upande mwingine lakini kwa upande wa Mji mwema kimya kilitanda kupita maelezo. Mpishano wa vijana ulikuwa mkubwa huku shughuli za kawaida za kila siku zikiwa zinaendelea. Kwa umbali wa kama mita 100. Unaonekana mwanga kama wa kurunzi kubwa yenye kufifia kiasi, mwanga huo ulionekana ukijongea taratibu kutokea mbali kuja sehemu ambayo kidogo kulikuwa na changanyikeni ya watu. Kadiri mwanga huo ulivyokuwa ukijongea kuufuata mwanga wa taa nyingi za umeme zilizosimikwa kwenye kuta ya majengo kadhaa ya hapo mtaani, ndivyo taa ile ilivyoanza kugundulika kuwa ilikuwa ni ya kitu gani na ilipokaribia ndipo ikajulikana kabisa. Ilikuwa ni baiskeli kubwa aina ya Phonix ya kizamani ambayo ilikuwa ikiendeshwa taratibu na kwa uangalifu mkubwa, mtu huyo akazidi kuinyonga baiskeli yake hadi alipofika kwenye kijiwe cha Kahawa ndipo akabana mikono ya breaki na kupunguza mwendo hadi aliposimama kabisa.




"Dokta unatokea mjini na baiskeli leo?" Akauliza mzee mmoja aliyopo hapo kijiweni katika harakati zao za kimazoea za kujipatia Kahawa.




"Siku mojamoja napunguza mafuta mwilini kwa mazoezi siyo kila siku pikipiki tu mwili unadumaa." Akajibu Dokta Gabriel Nyagile akiwa anapiga hatua ndogo ndogo kuitafuta nafasi ya kujichomeka.




"Mjini kwema lakini?" Akauliza mzee mwengine wa pembeni ya muuza kahawa.




"Mjini kwema tu, ni mihangaiko ya hapa na pale bwana hakuna ziada." Akatulia kidogo kisha akasema.




"Hebu niwekee Kahawa ya moto Kwetu kaya hata hivyo usinipunje bwana,"


Kahawa ikawekwa mezani na kusogezewa mbele yake.




"Na Kashata?" Akauliza muuzaji ambaye kwa jina la mazoe walipenda kumuita Kwetu kaya.




"Mgosi nani asiyejua kuwa umekuja hapa kwa waluguru kuja kusakanya pesa lakini usiwe msahaulifu kwa wateja wako, tangu lini mimi nikanywa Kahawa na kashata." Akaongea Daktari huku akikitwaa kile kikombe kidogo cha Kahawa na kukipeleka kinyawani. Ulikuwa ni mwendo wa Kahawa na soga, soga na Kahawa. Hoja mbalimbali zikaundwa, michezo mbalimbali hasa mchezo maarufu wa mpira wa miguu mabishano yakaamka huyu akisema hivi yule anakuja na hoja hii. Huyu akiipa sifa timu hii yule anawapamba wachezaji wa timu yake. Mara ikafa ikaja mada ya sifa kwa wanawake hapa mada ikakolea hata hivyo mada hii ilimkuta Daktari Gabriel akiwa ameshatandika vikombe vyake vitano vya Kahawa na hitaji lake kufika tamati akasimama na kutoa noti ya shilingi Elfu moja na kumkabidhi Mgosi au Kwetu kaya ambaye aliipokea kwa bashasha.




"Nimekunywa vikombe vingapi?" Akauliza Dokta Gabriel.




"Umekunywa vikombe vitano halafu nashangaa leo hukuja na chupa yako ya kubebea Kahawa?"




"Nimeshaijua dhamira yako Mgosi, nia na madhumuni isibaki hata ya ubuyu kwa watoto wa mtaani kwangu, haya hiyo mia tano iliyosalia watagawana wazee wangu hapa lakini usisahau kumpa kikombe kimoja kijana wangu Athumani hapo mzee wa Simba damudamu." Akamaliza kuongea Dokta Gabriel kisha akageuka kuifuata baiskeli yake huku akizipokea shukurani za aliowaachia oda ya Kahawa.




Saa nne kasoro robo ilimkuta nyumbani kwake akiwa tayari ameshafanya kila aina ya purukushani, alikuwa amejikalisha barazani kwake kwenye kiti cha kusuka kwa magamba za Mianzi akiifunua Dunia kwa kurasa kadhaa hasa mpya zilizomzukia siku nzima akiwa kazini. Alijaribu kuwafikiria wageni waliyomjia kwa mapana zaidi kisha kuwachambua na kuwatafutia tabia.




Wote walikuwa ni wanausalama lakini yule mwanamke sijui kwa nini alibeba upole na ucheshi halafu wale wengine watatu wanaume wawe wakali na wenye lugha za kutishia amani? Aliwaza Dokta Gabriel Nyagire. Akiwa hapo akajishauri mengi na kujikosoa hili na lile hata hivyo akapata tabia za ujumla za wanausalama zilivyo. Kubwa ilikuwa ni kutokutabirika wanakuja au watakujia kukuhoji kwa namana gani, pili ikiwa ni namna wanavyoweza kujibebabeba kama marafiki na muda mwingine sura za kirafiki kuzitia mfukoni na kuweka roho mbaya ya kutesa na kuuwa kabisa kama wakishindwa kufikia muafaka na wewe. Hizi zilikuwa ni tabia za wanausalama alizozijengea picha kichwani mwake kwa uwezo wake wa kufikiri na kujua baadhi ya mambo. Akaiwasha simu yake ya mkononi kutazama majira Mh! Akagumia mara baada ya kuona majira yalivyokuwa yakizidi kuyoyoma na kukaribia kuuita usiku mkubwa. Ilikuwa imegota saa tano na nusu usiku. Akajinyanyua kivivu na kukibeba kile kiti na kukisogeza pembeni kisha akanyoosha mgongo, uzee ulikuwa umenza kumtesa sasa kwani alipojinyoosha viungo vyote vya mwili vilimcheka na kumdhihaki. Akiwa anaunyoosha mgongo wake akaona kivuli kikikatiza kona moja na nyingine akashtuka hata hivyo alipuuza na kuhisi huwenda ni macho yake mabovu yalimtengenezea zengeu. Akapiga hatua ndefu akaufikia mlango na kuingia hata hivyo kabla hata hajaufunga mlango kwa funguo ukasukumwa kwa ndani kiasi cha kumpiga kikumbo kidogo kumrudisha nyuma.




"Nani jamani tena?" Akauliza akiwa na hofu sana.






Akiwa anaunyoosha mgongo wake akaona kivuli kikikatiza kona moja na nyingine akashtuka hata hivyo alipuuza na kuhisi huwenda ni macho yake mabovu yalimtengenezea zengeu. Akapiga hatua ndefu akaufikia mlango na kuingia hata hivyo kabla hata hajaufunga mlango kwa funguo ukasukumwa kwa ndani kiasi cha kumpiga kikumbo kidogo kumrudisha nyuma.




"Nani jamani tena?" Akauliza akiwa na hofu sana.




"Ni mimi mzee wangu nimependa kukutembelea nyumbani kwako leo au hupendi wageni?" Mgeni asiyeeleweka akajibu kwa utulivu mkubwa akionekana akihema sana mithili ya mtu aliyekuwa akikimbia mbio zenye urefu fulani. Alivaa kiajabu ajabu sana.




"Si kwa utaratibu huu lakini ni nani wewe?" Akajibu Dokta Gabriel Nyagile na kuuliza kwa wakati mmoja.




"Ni mgeni niliyependa kukutembelea usiku huu?" Akajibu huku akipiga hatua hadi katikati ya sebule ile ambayo haikuwa na vitu vingi sana vya thamani, kulikuwa na meza kubwa tu ya mti wa Mfenesi, stuli tatu zilizoizunguuka ile meza. Juu ya meza hiyo kukiwa na kitabu kikubwa cha riwaya ya mwandishi wa ki-Marekani iliyoandikwa na Sidney Sheldon inayokwenda kwa jina la The other Side of Midnight, kulikuwa na chupa kubwa ya maji safi ambayo ilibakiwa na maji nusu sambamba na vikorokoro vingine. Wakati mgeni huyo asiyeeleweka aliyevaa nguo ya moja kwa moja mfano wa ninja au Spider man huku juu ikiwa imefunikwa na koti jeusi refu lililokuwa likikaribia kugusa sakafu ya pale sebuleni, miwani ya rangi nyeusi ambayo haikuhofia nyakati zile za giza sambamba na viatu vyeusi kama vya kijeshi vilivyopanda hadi ugokoni vyenye chuma mbele, akiwa anaikagua ile sebule, Dokta Gabriel alihisi hatari imemvamia nyumbani kwake akaamua kulivuta pakiti la sigara kutokea kwenye mfuko wake wa shati ambalo hakuwa amelifunga vishikizo ili kuuruhusu upepo ulipepee tumbo lake wakati akiwa barazani akiisimanga dunia akilini mwake. Akatoa sigara moja na kuipachika kwenye kingo zake za mdomo na kuiwasha kwa kiberiti cha gesi ambacho aghalabu kilikaa sambamba na ile pakiti ya sigara. Ule mwanga ukamgutusha yule mgeni ambaye alikuwa amempa mgongo Dokta Gabriel kwa kiasi fulani, akageuka kumtazama mzee huyo kisha akakenua tabasamu la kejeli.




"Dokta Gabriel Nyagile, mtaalamu wa magonjwa ya moyo na upasuaji," yule mgeni wa ajabu asiyeeleweka aliuvunja ukimya ulioanza kuomba uwenyeji sebuleni hapo huku akizirusha hatua zake kwa madaha akiizunguka ile sebule akaendelea.




".....mguu huu wako, nimeona....nimeona jinsi wanausalama wanavyokuandama na kutaka kujua kitu kutoka kwako, nimeona hatari ya siri zetu kuvuja na kutufelisha ama kutuzuia tusifikie lengo. Tambua kuwa huu ni mpango kabambe, mpango ambao hautakiwi kufeli kwa sababu unamalengo makubwa sana ya kuhakikisha tunafika pale ambapo ndiyo lengo hasa la mpango huu. Ingawa si hapa nchini kwenu hata hivyo kama hatuta safisha huku ni wazi kazi inaweza kuwa ngumu kwetu. Nimeona jinsi walivyokuja mchana na kukuhoji kisha wale waliokuja majira ya alasiri pia wakakuhoji. Sitaki kujua walikuhoji nini wala sitaki kujua uliwajibu nini," akaweka koma mtu huyo kisha akaisogelea meza na kukaa kitako juu ya ile meza akiwa mtulivu kabisa. Dokta Gabriel akaivuta sigara yake kwa pupa kisha akaumeza moshi wote kama ni sehemu moja ya kutoa dukuduku la hasira kwa siku hii ambayo hadi inaisha bado ni tafarani. Akaichukia siku yote na kuilaani kabisa.




"Unataka nini sasa?" Akahoji kwa hasira huku jicho likiwa jekundu kama nyanya ya masika ikiwa ni matokeo ya kuumeza ule moshi wa sigara.




"Nimekuja kukufumba mdomo ili usisumbuliwe tena na wanausalama....unajua wanausalama ni wasumbufu sana, watataka kuja kila siku ili tu uwape majibu wanayoyataka na huwa ni kama wachawi maana ni wepesi kuutambua uwongo na ukweli. Kuepuka hilo nimeona nije kukuweka mbali nao ili uishi kwa amani bila kuwaona wala wao kukuona." Akajibu yule mgeni sasa akipeleka mkono kwenye kiuno chake ndani ya koti na kuchomoa bastola iliyofungwa kiwambo cha kuzuia sauti mapema. Macho yakamtoka pima Dokta Gabriel Nyagile huku ile sigara ikimtoka mkononi na mwili kuanza kumtetemeka.




Kwanini afe? Akajiuliza. Jibu likachelewa kuja hata hivyo pia hakupata muda wa kujifikiria hata namna ya kujibu, kasiba ya bastola ile ikamuelekea na risasi moja kamilifu ikajaa kifuani mwake na kwenda kumrusha kwa nyuma na kumbwaga sakafuni damu zikiwa zinatoka kwa fujo mara baada ya moyo wake kufumuliwa vibaya kwa risasi hiyo iliyotokea kwa nyuma. Kimya kikamkumba Dokta Gabriel Nyagile na hakikuwa kimya kidogo bali kilikuwa ni kimya cha kifo kilichomnyima hata nafasi ya kukunja na kunyoosha miguu. Dokta Gabriel akawa wa baridi masaa machache mbele huku muuaji asiyefahamika akipotelea gizani.


Aliuawa.




Waswahili husema kumekucha na makucha yake, hakika siku hii iliyofuata ilikucha na makucha yake makali ambayo kila mmoja alijawa na sintofahamu juu ya kile kilichotokea. Ilikuwa ni asubuhi ya Tanzia, asubuhi iliyopambwa na taarifa tata ya kifo cha Dokta Nyagile. Majirani walijazana nyumbani kwake kushuhudia kile kilichotokea asubuhi hiyo nyumbani kwa Daktari huyo. Vijana watatu waliyokuwa wamepanga kuondoka mjini Morogoro na kuelekea jijini Dar es salaam waliamua kuivunja safari hiyo na kuwa wa kwanza kufika kwenye tukio baada ya taarifa ya kifo hicho kuzipata mapema kwenye taarifa ya habari. Wakawahi nyumbani kwa Dokta Nyagile na kukuta umati wa watu ukiwa umesongamana katika vikundi vidogovidogo huzuni ikiwa nao. Sembuyagi akawa ni wa kwanza kujipenyeza na kutokea kwenye eneo lililokuwa na vijana kadhaa wakijadili hili na lile.




"Habari zenu?" Akasalimia Sembuyagi akiwa macho juu juu hajatulia.




"Kama unavyoona ndugu yangu hali si hali mzee wetu bwana!" Kijana mmoja akajibu akiwa na huzuni.




"Ilikuwaje?" Akaongeza swali.




"Hakuna anayejua ilivyokuwa sisi taarifa tulizipata kutoka kwa kijana anayemletea maziwa kila siku asubuhi, kijana huyo aliukuta mlango uko wazi kwa maelezo yake sasa huwa kwa kawaida akiukuta mlango ukiwa wazi huingia na kuweka chupa ya maziwa mezani sebuleni na kuondoka. Alipoingia ndani baada ya kuusukuma mlango, alichokikuta ilibidi apagawe na kupiga kelele huku akitoka nje ikatubidi sisi tuishio karibu na mzee wetu tuwahi. Tulikuta kitu cha namna ya ajabu sana, kilikuwa ni kifo cha kutisha na moja kwa moja tukajua ni risasi." Alitoa maelezo kijana mwengine wa pembeni.


ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog