Search This Blog

Saturday 5 November 2022

MAGNUM 22 - 4

 






Simulizi : Magnum 22

Sehemu Ya Nne (4)





USIKU WA MANANE

SIKU HIYO HIYO

Wakiwa wote wamelala, Kamanda Amata alitembea taratibu koridoni na kuelekea chumba maalumu chenye kila takataka ya mawasiliano, mkononi mwake alikuwa na vitu vitatu tu; kijitabu kidogo cha kumbukumbu, na kipande cha noti na mkanda wa kiunoni aliyopewa kule kaburini. Akaviweka mezani na kuchukua kile kijitabu cha kumbukumbu na kuanza kukisoma kurasa moja baada ya nyingine, lugha iliyotumika kuandika kumbukumbu hizo ilikuwa tatanishi, sehemu nyingine akaelewa na kwingine kukapita.

Hata huyu naye alikuwa anamsaka Martin Gupter! Akawaza na kuendelea kupekua kijitabu kile chenye mambo mengi. Katikati ya kijitabu kile akakutana na namba ambazo hazikuwa zikieleweka, akazikodolea macho asijue hata ni nini maana yake, akaanza kuingiza moja baada ya nyingine kwenye kompyuta lazkini hazikumpa maana, akaachana nazo na kuendelea kusoma vitu vingine. Kila alipokuwa akisoma kuna baadhi ya vitu alikuwa akiviandika pembeni kwenye karatasi nyeupe mpaka aliporidhika. Akaichukua ile noti na kutazama vizuri.

Kipande chake kiko wapi? Akajiuliza, akaona haina haja kuumiza kichwa maana si rahisi kujua, akajiegemeza kitini na kupitiwa na usingizi mzito.

* * *

Asubuhi kulipokucha akajikuta bado yupo palepale amekarti na kila kitu kiko vilevile, “Usingizi hauna adabu!” akajisemea kwa sauti ndogo na kukichukua kile kijitabu na kuendelea kurasa nyingine za mbele. Karibu na kurasa za mwisho akakutana na kifungu cha maneno ambacho kimezungushiwa kama kiboksi hivi kwa kalamau ya wino, na katika kifungu hicho kuna herufi zilizchanganywa na tarakimu na alama nyingine nyingine.

“Identity!” akajisemea, kwa kuwa alielewa kuwa huo ni utambulisho wa mwenye kijitabu hiko. Kamanda Amata akshusha pumzi kwa maana zaidi ya kusikia kikohozi na chafya na kuhisi mshiko wa mkono wa marehemu, hakuwahi kumwona sura mtu huyo kutoka na giza nene na zito ndani ya kaburi lile.

“Ni nani huyu?” akajiuliza huku akiinuka na kuiende kompyuta kubwa iliyo ndani ya chumba hicho akaiwasha. Mara nyingi kompyuta hii hutumiwa na Chiba katika maswala ya utambuzi na kadhalika. Akiwa katika kuiweka sawa ili afanye kazi yake, akasikia mlngo ukifunguliwa, akageuka na kukutana macho kwa macho na Chiba.

“Kamanda vipi?” Chiba akamuuliza.

“Kuna kitu nataka nikitambue hapa, sasa nimeona kukusmbua si fresh..!” akajibu.

“Aaaah, kitendo tu cha kuiwasha hiyo kompyuta mimi kule nimejua ndiyo maana nikaamka kuja kutazama kulikoni, isije kuwa tumevamiwa na mchwa,” Chiba akajibu huku akiwa tayari kafika eneo lile.

“No! si hivyo, ingiza hapo … enheee, sawa, bofya hapo kwenye scan … yes! Sasa subiri!” Chiba akamwelekeza Kamanda jinsi ya kufanya baada ya kugundua kuwa amekose katika kuingiza hizo. Baada ya dakika kama mbili hivi, Amata akajikuta katokwa na macho na kupigwa bumbuazi kwa maelezo yanayokuja juu ya kioo kile.

“Unamjua?” Chiba akauliza.

“Yes!” Amata akajibu, “Namjua vyema, huyu bwana anaitwa Costantine, ndiye niliyemwokoa dhidi ya mkono wa Pereira kule Angola, huyu naye kama mimi alikuwa katika harakati za kumsaka Martin Gupter… aisee, Costantine amekufa!” akaongeza kusema kisha chozi likamdondoka.

Chiba akampigapiga begani huku naye akisoma maelezo yaliyojitokeza katika kifaa hicho.

Mpelelezi binafsi! Akawaza.

Amata akainua kichwa na kutulia kimya, “Ni vipi kama asingekuwa yeye, ningekuwa hai leo? Si kwamba nalia kwa sababu amekufa, no, kufa ni ratiba ya kila mja, ila ninalia kwa sababu nakumbuka maneno ya wahenga ‘wema hauozi’,” akamwambia Chiba kisha akaendelea kusoma maelezo yale vizuri na kumjua vyema rafiki huyo aliyemtoroka kule Angola..

Alikuwa anajua ni wapi Gupter anapatikana! Akawaza huku akiendelea kuchambua yale maandishi na mwisho wa yote akakutana na ramani ndogo, akaitazama vizuri na kuielewa akisaidia na Chiba.

“Hii ni ramani ndogo ya Waterloo!” Chiba akamwambia Kamanda Amata.

“Ina maana Costantine alitumia ramani hii kufika mahalia haswa alipo Martin Gupter!” Amata akamwambia Chiba huku akiiprinti ramani ile katika karatasi. Alipohakikisha anayo tayari mkononi, akaendelea kuchambua kama atakutana na vingine vya kumfaa. Alipojiridhisha kuwa hakuna akafunga kompyuta na kubaki katulia kimya huku kile kijitabu kikiwa mkononi mwake pamoja na kile kipande cha noti.

“Bado nitajua moja baada ya jingine!” akasema huku akitoka ndani ya chumba kile na kurudi katika chumba chake cha kulala na kujibwaga kitandani akiwa na mawazo mengi.



WATERLOO

Katika jumba kubwa lililotengwa na makazi ya watu na kujengwa mbali kidogo ila pembezoni mwa Mto Lofa, Martin Gupter alikuwa na kikao cha dharula na swahiba wake yaani Amanda na Fredy. Aliwaita kwa mazungumzo mara baada ya kupata ujumbe kuwa sasa anasakwa kwa udi na uvumba kila kona ya Afrika.

“Tupo matatani,” akawaambia, “kuna timu ya wapelelezi imesambazwa, Angola, Tanzania na Ivory Coast kwa ajili ya kutusaka,” akaongeza.

“So?” Fredy akauliza.

“Lazima tuwe na tahadhari kubwa sana tutokapo nje, tuwasome kila tunaowaona, tutakayemtilia shaka tu lazima tumtie mkononi,” akamjibu.

Ukimywa sekunde kadhaa ukajidai katikati ya watatu hawa.

“Sina wasiwasi!” Amanda akasema.

“Kwa nini?” Martin akauliza.

“Kama kuna mtu nilikuwa na mwogopa na kumhofu ni huyu wa Tanzania, kwa sababu ni yeye tu ambaye tunaweza kusema tumepambana na anajua wapi tupo,” akasema.

“Aaaaah huyo anongea na babu zake saa hii…”

“Kama ni hivyo, siwezi kuviogopa vimburu vingine hivi, vikimtia mguu hapa tunavitenganisha roho na mwili,” Amanada akajibu. Wakiwa katika mazungumzo hayo simu ikaita kwa nguvu na fujo, Martin akampa ishara Amanda akaipokee, naye akafanya hivyo.

“Yes!” akaitikia na kumsikiliza mtu wa upande wa pili.

“(…)”

“Ok, copy that!” akajibu na kukata simu kisha akaja kwa wenzake na kuketi pale pale alipokuwa ameketi mwanzoni.

“Vipi?” Martin akauliza.

“Subiri nukushi inaleta habari sasa hivi, nafikiri inabidi tufanye hesabu za kuto sasa,” akawaambia na sekunde chache tu, mashine ya nukushi ikapata uhai na kuanza kupiga kelele zilizofuatiwa na karatasi kama mbili hivi. Amanda akainuka tena na kuziendea, akazinyofoa na kurudi nazo kitini, akampa Martin kuzisoma.

… najua kuwa mna miezi miwili ya kumaliza kazi yenu, hapa nataka kuwapa nafasi nyingine pekee ambayo mnaweza kuitumia kukamilisha kazi yenu kabla ya wakati na kupokea pesa zenu mbaki mnatwanga maisha mtaani.

…Kutakuwa na kikao cha dharula katika Jiji la Addis Abbaba, kikao hiki kita kitahuduriwa na marais wachache na viongozi wengine wa Baraza la Usalama, lengo ni kufanya tathmini ya uchunguzi wao na pia wanataka kutoa tamko la mwisho juu ya mzozo huu wa Somalia.

… kwa hiyo kuna mambo mawili, ama wakubaliane na matakwa ya Jaffery Bakhar au wakatae, tayari wamemtumia taarifa ya yeye kufika Addis kwa ajili ya mazungumzo ya swala hilo. Je; mwaweza kuitumia nafasi hiyo?

Pamoja na maelezo mengi, haya nayo yalikuwa ndani ya nukushi hiyo. Martin akashusha pumzi na kuwapa wenzake ile karatasi nao wakaisoma kwa zamu. Baada ya wote kumaliza ikawekwa mezani.

“Vipi, tutumie nafasi hii?” Fredy akauliza.

“Siku saba zinatosha kufanya maandalizi? Maana mkumbuke kupanga mashambulizi si kitu kidogo!” Amanda akasema.

“Huu ni mchezo wa hatari sana, kwa nini wamemwita Bakhari? Siyo mtego huu?” Martin akawauliza wenzake, “isije kuwa wanataka kummaliza ili kelele hii iishe,” akaongeza kusema.

“Hapa kuna utata, tunaweza kwenda tukatiwa mbaroni kirahisi sana,” Fredy akasema.

“Acha uoga Fredy, tuitumie nafasi hii, inaweza ndo ikawa bahati pekee kwetu, na ninafikiri, safari hii sintotumia bunduki kuua…”

“Utatumia nini?” Amanda akauliza.

“Siwezi kukwambia ila utajua mtu atakapokufa,” Martin Gupter akawaambia swahiba zake.

“Hapo ndipo ninapokupendea, hupendi kuweka wazi mipango yako…” Amanda akamwambia Gupter.

“Nilizoea kutumia bunduki moja tu, na nimeishi nayo miaka kama ishirini hivi, ilikuwa kama mwanangu, na imenifanyia kazi nyingi sana, sasa mshenzi yule akafanikiwa kuitoa mikononi mwangu… nina kazi ngumu ya kupata nyingine kama ile, kwa sasa nitamaliza kazi zangu kwa mikono na sumu tu basi,” Martin akasema.

Martin Gupter katika kazi yake yote ya mauaji aliizoea sana bunduki hii ‘Magnum 22 riffle’, haikuwa maalumu ya kudungulia ila yeye alipenda kuitumia kwani aliiamini kuwa ina nguvu za kutosha katika kummaliza adui yake. Haikuwahi kutoka mikononi mwake kwa takribani miaka ishirini lakini sasa ni Kamanda Amata aliyeharibu utaratibu huo na kufanikiwa kuipata bunduki hiyo kisha kuihifadhi Shamba. Japokuwa ilikuwa ni pigo kwake, bado Gupter aikuwa mtaalamu sana katika maswala ya uuaji, aliweza kuua kwa mitindo mbalimbali na kwa ustadi wa hali ya juu sana na ndiyo maana alikodiwa na watu mbalimbali waliotaka kutekelezewa kazi kama hizo.

Martin Gupter alikuwa kwenye orodha ya watu hatari, akioneshwa na CIA kwa sura kama hamsini tafauti, akinaswa kwa sauti nyingi tafauti, MOSSAD walimwelezea kama Shetani mwenye bunduki ya kizamani, kila shirika la kijasusi ambalo ndani ya nchi yao kijana huyu keshafanya maangamizi walimpachika jina wanaloona linamfaa. Aliamini kuwa kwa kuweza kuzitoroka ngome ngumu kama hizo za kijasusi za Ulaya na Mashariki ya mbali asingeweza kutikiswa na Afrika, alijua atachukua kazi na atamaliza kwa wakati bila hata kipingamizi. Kila anapokwenda alikuwa na timu yake anayoiamini sana, Amanda na Fredy, wao nao kama makachero watoro kwenye nchi zao walimsaidia vyema sana Martini kuweza kufanikisha mauaji yake katika ngome yoyote ile duniani.

Haikuwa mara ya kwanza kwa Jaffery kumpa kijana huyu kazi, alimwamini na ndiyo maana hata safari hii, kwenye kazi ya kuipigania nchi yake alimtafuta na kumfanya kama kifaa cha kuushinikiza Umoja wa nchi za Afrika kuigawa Somalia vipande viwili ili Kusini kutawaliwe na tajiri huyu kwa madai kuwa ni ardhi ya mama zake.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Tunaingia kazini! Ngoja niwasiliane na tajiri, ila jiwekeni tayari,” Martin akawaambia swahiba zake huku akiiendea simu ya mezani na kupiga namba fulani, akaweka sikioni kifaa kile na kusikiliza upande wa pili. Baada ya mazungumzo kama ya dakika kumi na moja hivi akakata simu na kurudi kwa wenzake.

“Jaffery anasema tutumie nafasi hiyo kama loope hole ya kuwamaliza, ila sharti lake ni lile lile, asipokuwepo yeye basi atamtuma binamu yake kwenda kwenye kikao hicho na kuwa msemaji badala yake. Wakikubali matakwa yake basi tuweke silaha chini, wakikataa tutekeleze mbinu ya mwisho na tayari jeshi litaivamia Somalia na kuendesha vita isiyo na mwisho…” Martin akaeleza.

“Sasa nimepata mbinu, tunachotakiwa kufanya ni kuwa pale lakini kuwa wapole sana, hata kikao kikiisha sisi tusifanye lolote ili Martin utekeleze kazi yako kimyakimya nasi tutakulinda,” Fredy akaongeza.

“Ndiyo, na huo ndo ujanja sasa ambao nataka tuutumie. Unajua wataimarisha ulinzi, wakijua tupo, sasa sisi hatutumii nguvu sana kama mwanzoni, mlengwa wetu ataamka akiwa marehemu basi!” Martin akawaeleza.

“Kwa hiyo!” Amanda akatamka.

“Tuingie kazini, siku saba kabla, yaani ikiwezekana kesho Amanda utangulie au mjipange wenyewe,” akawaambia.







SEHEMU FULANI HUKO SOMALIA

KIKOSI cha vijana kama elfu moja waliovalia nguo za kijeshi na kujifunga vitambaa vichwani mwao na wengine wakiwa wamevaa soksi usoni, kila mmoja alikuwa na bunduki kubwa ya kisasa yenye nguvu mkononi mwake, walikuwa wamesimama kimya katika vikosi vya watu mia moja mia moja huku kila kikosi kikiwa na bendera nyeusi. Licha ya kuwa na silaha hizo nzito, kila mmoja alikuwa na sime kiunoni mwake.

“TUNAUTAKA UMOJA WA NCHI ZA AFRIKA KUIGAWA JAMHURI YA SOMALIA NA KUWA NCHI MBILI HURU!” alisikika mtu mmoja aliyekuwa amesimama mbele yao juu ya kijukwaa kidogo, akiwa na kipaaza sauti mkononi mwake.

“MAZUNGUMZO YA MWISHO YATAFANYIKA WIKI MOJA IJAYO, HIVYO WAKIKUBALI, ARDHI HII TULIYOSIMAMA ITAKUWA NCHI YETU, WAKIKATAA TUTAANZISHA VITA ISIYO NA MWISHO!” akawaambia na wao kwa kutii agizo hilo, wakainua bunduiki zao na kupiga risasi juu mara tatu.

Baada ya taarifa hiyo wanajeshi hawa wakatawanyika na kuingia katika maficho yao ya kila siku. Fadicky Al – Habib aliteremka kwenye kile kijukwaa na kuvuta hatua huku akifuatwa na vijana wengine wanne ambao nao walivalia kijeshi kama wale wanajeshi.

“Unafikiri watakubaliana na matakwa yetu?” mmoja wa wale vijana akamuuliza.

“Wasipokubali ndipo watakuwa wamefungulia bomba la damu katika ardhi hii,” akasimama na kumwambia yule kijana, “Jaffer anahitaji kitu kimoja tu, ardhi ya mama zetu, hivyo wasipoitoa kidiplomasia wataitoa kwa mtutu wa bunduki,” kisha akaendelea kutembea na kuingia ndani ya hema ndogo yenye ulinzi mkali kwa nje. Wakaketi katika zuria kubwa na la kisasa, wanadada wawili warembo wakapiga magoti huku na huku wakimkandakanda mabega.

“Yusra, jiandae, weka watu wako vizuri, siku isiyojulikana tutaondoka hapa kuelekea Addis!” akamwambia yule kijana.

* * *

DAR ES SALAAM

OFISI YA MUDA YA BARAZA LA USALAMA LA A.U

Kikao cha wajumbe wale wale kilikutana tena katika afisi hii iliyoteuliwa kuhifadhi nyaraka zote za kiusalama kwa kipindi hiki. Usiku huu kama walivyoitwa na Mwenyekiti wa baraza hilo walifika na akidi ilitimia. Madam S alikuwa ameketi katika kiti chake kile kile na wajumbe wengine nao vivyo hivyo.

“Kama tulivyoelekezana kuwa kwa kazi hii tutaitana muda wowte hata kama ni usiku wa manane kama leo hii … nimekuitena kwa sababu kuna jambo ambalo limejitokeza na lazima lifanyiwe kazi. Kikao cha dharula cha wadau wa AU baada ya kukutana jana pale Addis, kimeamua kwamba ufanyike mkutano wa mazungumzo kati ya AU na huyu Bwana Jaffery Bakhary ili kufikisha mwisho mgogoro huu…” akalieleza jopo hilo ambalo lilikuwa kimya kabisa likifuatilia nini mkuu huyo anataka kusema.

“Hivyo basi siku saba zijazo kutafanyika kikao hicho ndani ya ukumbi mdogo wa mikutano katika jingo letu la AU Headquaters. Dhumuni la kikao hiki sasa ni kwamba sisi kama baraza la usalama la jumuia hii tunatakiwa tuandae ullinzi wa kutosha kuwalinda viongozi wetu siku hiyo. Sasa nakaribisha mawazo yenu ni jinsi gani tutaweka ulinzi eneo hilo,” akamaliza na kuzima kifaa chake cha kuzungumzia.

“Tupo kwenye harakati za kuwasaka hawa jamaa wanaofanya mauaji ya viongozi … sasa na tena tunaandaa kikao cha viongozi hao hao, Mwenyekiti huoni kama tunaweza kuwa tunarahisisha kazi kwa wauaji kutekeleza mpango wao?” mjumbe mmoja akauliza.

“Lakini je, huoni kuwa inawezekana kuwapata wauaji kirahisi kama watakuja mahalia hapo, na najua kwa vyovyote watakuja kwa sababu ni wafuasi wa mtu huyu, nsiyo maana nataka tujadiliane jinsi ya kuweka ulinzi huu na kuhakikisha tunamtazama kila mtu,” yule mwenyekiti akasema. Ukimya ukajidai kwa nukta chache kisha mjumbe mwingine akakohoa.

“Kwa hiyo tunafanyaje? Vijana tuliowasambaza tunawarudisha na kuwapeleka Addis au tunaunda kikosi kazi kingine?” mwingine akauliza.

“Ndiyo nataka tuone pamoja kama tunawapa kazi hawahawa au hawa tuwaache na misheni yao kule waende wengine…. Tuweke mawazo pamoja!” mwenyekiti akaeleza.

“Mjue mnapambana na nani!” Madam S akawaambia, “wale au yule kama ni wauaji au muuaji mwenye profesheno yake katika kazi msifikiroi atajileta kirahisi hivyo au atatumia mbinu ile ile. Tazameni alivyoua Angola sivyo alivyoua Ivory Coast … alipojaribu kutumia mbinu ileile hapa Tanzania tukampa ambush ya nguvu hata silaha yake akaicha hapa, sasa unafikiri kama atakuja Addis atatumia mbinu hiyo hiyo?” akawaacha kwa swali.

“Sure! Anachosema Madam pale ni sahihi kabisa, inabidi tutanuke na tunuse katika kila kitu ikiwezekana tupenyeshe watu wetu kwenye kona zote muhimu, ili waangalie kila kitu kwa ukaribi zaidi…” mjumbe mwingine akasema.

Kikao kikaendelea na mipango mingi ikasukwa kwa ajili ya siku hiyo, wakatakiwa kukusanya wana intelijensia kutoka sehemu tafauti za Afrika ili kuwapenyeza kwa siri katika Jiji hilo kuweka usalama. Lakini katika uteuzi wote huo haikuguswa idara nyeti ya TSA, kwa kuwa ilisemwa kuwa Tanzania imeshindwa kuongoza operesheni hiyo tangu awali, hata Madam S alipotaka kutetea hilo hakusikilizwa,”

“Kwa kuwa hawa washenzi walitaka kutekeleza mauaji ndani ya nchi hii, vijana wangu wataendelea kuwasaka popote walipo katika dunia hii bila kujihusisha na kikosi cha AU…” Madam S akazungumza kwa hasira.

“Sasa mjumbe kutoka Tanzania, kumbuka kijana wako unayemtegemea sana mpaka sasa hajulikani alipo, utampelekea nani tena huko, hili swala liache, tutalifanyia kazi kama kamati…” mwenyekiti akasema.

“Sina kijana mmoja, ninao zaidi ya mia tano wazuri kuliko yule. Ninachotaka nikwambie ni kwamba, siridhiki na mwenendo wa kamati hii, kuna ulakini hapa, leo sintosema lakini nitakuja kuwaambia bado nafanya uchunguzi wangu… si ajabu kuna watu au mtu anajua kila kinachoendelea lakini anajifanya msafi…” Madam akazungumza huku tayari anataka kuondoka.

“Mjumbe, naomba utangue kauli yako… ina maana humu ndani kuna msaliti, unamaanisha hivyo? Yaani sisi wenyewe ndiyo tufanya mauaji ya viongozi wetu?” akaongea kwa ukalia.

“Mi sijasema hivyo, ila hayo umesema wewe…”

“Wewe lazima ushughulikiwe, we mwanamke wewe lazima ushughulikiwe na kamati ya nidhamu,” Mwenyekiti akaongea huku kijasho kikiwa kinamtoka, akaketi na kushuhudia mwanamke huyo akiishia nje ya jengo.

“Aaaaaaggghhhh!!!! Ameniuzi kabisa bullshit!” akang’aka na kuinuka kitini, akaingia katika mlango mwingine na kujifungia maliwato kwa dakika kadhaa, kisha akarudi kuungana na wengine na kikao kikaendelea.

* * *

USIKU HUO HUO

Katika makutano ya Barabara ya Morogoro na Bibi Titi, Madam S alikuwa akikatisha usiku huo kuelekea ofisi ndogo. Mara kutoka barabara ya upande wa pili alisikia sauti kali ya gari, akageuka na kuona Land Rover nyeusi ikiwa mita mbili kutoka kwake, kabla hajafanya lolote, kishindo kikubwa kikasikika. Lile Land Rover likaipamia gari la Madam S na kulisukumia pembeni, likatupwa na kubingirita upande mwingine, lile Land Rover likakaa barabarani vizuri na kuendelea na safari kwa kasi kuelekea upande wa Mahakama ya Kisutu.

Usiku huo kulikuwa na watu wachache sana barabarani, hawakuzidi hata kumi, wakawahi kufika katika lile gari na kushuhudia uharibifu mbaya. Madam S alikuwa amebanwa na mkanda wa kiti alichokaa, hakuweza kutoka, damu zilikuwa zikimwagika kichwani. Kazi kubwa ilikuwa ni kumnasua mama huyo ili angalau wamweke pembeni apate upepo. Vibaka nao hawakuwa mbali aliyechukua simu akafanya hivyo aliyenyofoa redio haya.

Dakika kama thelathini baadae, gari la polisi likawasili eneo hilo, itifaki za kusalama zikaendelea na kumkimbiza mwanamama huyo Muhimbili, mpanga dakika hiyo hakuna mtu aliyemgundua majeruhi huyo.

Na huko Shamba TSA members walikuwa wakiendelea na shughuili zao, kila mmoja akiwa katika jukumu lake analopaswa kufanya. Simu ya mezani ikaanza kuita kwa fujo, haikuwa mbali sana na pale ambapo Chiba alikuwa ameketi.

Nani anayepiga hii simu? Akajiuliza huku akisukuma kiti chake kidogo ili kuifikia. Kila mmoja alishangaa kwa mwito huo maana simu hiyo inaweza ikakaa hata miezi miwili isitumike nah ii ni kwa sababu ni ya siri sana, njia zake zimefungwa kitaalamu kiasi kwamba haziingiliani na simu za kawaida. Ikiita ama inatokea Ikulu, Makao makuu ya Usalama wa Taifa na watu wachache wenye namba hiyo wasiozidi wane Tanzania nzima. Wote wakaikaribia wakati Chiba akiinyakuwa na kuiweka sikioni huku tayari kitufe cha kurekodi kikiwa kinafanya kazi.

“… umesema? … nheee…. Usiku huu au?” Chiba alionekana kuhamanika kwa simu aliyokuwa ameipokea. Baada ya hapo akakata na kuiweka mahala pake, akageuka na kukutana na macho nane yakimtazama.

“Vipi?” Amata akwa wa kwnza kuuliza.

Chiba hakujibu zaidi ya kuwatazama tu.

“Chiba nini?” Gina akadakia kuuliza.

“Madam S amepata ajali usiku huu kama saa moja au dakika arobaini na tatno zilizopita,” Chiba akawaeleza.

“What?”

Amata akang’aka na kuwaacha wenzake, dakika chache baadae akarudi akiwa keshavaa koti lake, “Simu imepigwa na nani?” akauliza.

“Inspekta Simbeye!”

“Smbeye?” akauliza na kuchukua simu yake, akapiga namba za inspekta huyo na kuzungumza naye machache kisha akaitua na kuitia mfukoni.

“Ok! Dkt. Jasmine, Scoba na Chiba nendeni Muhimbili haraka sana mkaweke mambo sawa, Mimi na Gina tunaenda eneo la tukio. Dakika ya tisini tuwasiliane,” Amata aatoa maagizo na kila mmoja akatawanyika tayari kwa kazi aliyopewa.



ENEO LA TUKIO

Gina aliegesha gari kando kando ya wigo wa Chuo Cha Ufundi Dar es salaam (Dar Tech) na wote wakateremka na kuelekea eneo hilo ambalo lilizungukwa na askari wa usalama barabarani na wale wa kawaida ambao walikuwa na silaha mikononi mwao. Amata na Gina wakawasabahi askari hao na kusogea pale lilipokuwa gari lile. Askari wenye silaha wakawazuia kwa kuwa tayari breakdown lilikuwa kwenye mchakato wa kuinua na kuivuta mpaka kituo cha polisi. Mazungumzo ya sekunde chache yakafanyika na Amata akaruhusiwa kusogea eneo lile, moja kwa moja akazunguka upande wa mlango wa dereva na kupenyeza mkono kwa upande wa chini, alipoutoa alikuwa na vitu viwili mkononi mwake; bastola ndogo ambayo haraka aliipachika kiunoni na kitu kingine kama pakiti la sigara lakini hiki kilikuwa cheusi, akakitia mfukoni na kutoka eneo hilo. Kando akakutana na askari mmoja mwenye sare nyeupe aliyekuwa na faili mkononi mwake na kuonekana akiandikaandika vitu fulani.

“Mmefanikiwa kuona gari lililosababisha ajali?” akamuuliza.

“Hapana! Inaonekana hawakusimama, kwani sisi tumefika kwa kuchelewa kidogo,” akajibu. Amata akatulia kidogo.

“Una undugu na huyu mama?” yule askari akamuuliza.

“Ndiyo, ni mama yangu…”

“Oh pole sana, wahi Muhimbili, hali yake sijui kama atapona,” sentesnsi hii ya mwisho iliufanya moyo wa Amata kupaa kwa hofu, haraka akarudi garini na kuketi kitini, akashusha pumzi ndefu.

“Vipi?” Gina akamtupia swali.

“Hali ya mama ni mbaya,” akajibu huku akichukua simu yake na kabla hajabofya namba yoyote ikaita, akaichukua na uiweka sikioni.

“Chiba!” akaita.

“Mama yupo mahututi,” Chiba akamwambia Amata.

“Nipo njiani kaka!”

Gina akawasha gari na safari ya Muhimbili ikachukua nafasi, “Ni ajalia au?” Gina akauliza.

“Siwezi kujua kwa sasa, lakini nitachekecha vizuri akili tutajua tu, hata gari iliyofanaya ajali itapatikana tu,” Amata akajibu wakati gari likiiacha Barabara ya Umoja wa Mataifa na kuchukua Mtaa wa Mindu kuelekea katika hospitali hiyo.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Hatua za harakaharaka zikawafikisha katika jengo la wagonjwa mahututi, wakaingia kadiri ya utaratibu wa wodi hiyo. Ndani ya chumba cha pekee Madam S alikuwa amelala kimya huku mashine ya oksijeni ikiwa puani mwake na ile ya kufuatilia mwenendo wa moyo nayo ilikuwa ikionesha mapigo hafifu. Daktari Jasmini alikuwa hima hima na madaktari wengine wakijaribu kufuatilia kila kinachoendelea kwa mgonjwa wao.

“Tunafanyaje?” Chiba akamuuliza Amata wakati tayari wakiwa nje ya jingo hilo, saa ya mkononi mwa Amata ilionesha saa nane usiku.

“Tutulie tu na tufuatilie kila kitu kwa ukaribu, ila kwa sasa tuzuie kila baya kama lipo, tutafanya hivi; Gina tunakuacha hapa na Scoba, muangalie usalama wa Mama kama mnahisi au mnamhisi yeyote kutaka kufanya baya, hakikisheni mnashughulikia. Madam S asiguswe na mtu yeyote kitandani iwe kuchomwa sindano au kufanyiwa tiba yoyote zaidi ya Dkt Jasmine, muwe macho. Mimi na Chiba kuna mambo tunayaweka sawa kisha tutawasiliana…” akatoa maagizo.

“Sawa, umesomeka mkuu…” Gina akajibu.

Chiba na Amata wakaingia garini na kutokomea zao. Breki ya kwanza ilikuwa katika kituo polisi kati, hapo wakakutana na Inspekta Simbeye ndani ya afisi yake chakavu ambayo hata haina mpangilio vizuri.

Mzee huyo aliyebwaga moyo wake kitini huku miguu yake mifupi ikiwa juu ya meza, aliwakaribisha wageni wake na kisha akaketi vizuri kwa mazungumzo.

“Tumekuvamia!” Amata akamwambia.

“Na nilijua mtakuja,” Simbeye akawajibu, “kwanza poleni sana kwa yaliyotokea…”

“Asante sana, tunasikitika sana na tunamhitaji huyo aliyefanya hivi, kwa akili yangu mbaya najua wazi kuwa si ajali ya kawaida,” Amata akamwambia Simbeye.

“Ndiyo, upo sawa, Kamanda … mnazungukwa! Naanza kung’amua kitu…” Simbeye akasema.

“Utu uzima dawa, nambie baba labda utaifungua akili yangu iliyolala,” Amata akamwambia simbeye huku akijiweka sawa kitini. Inspekta Simbeye, hakuzungumza kitu, akachukua simu yake na kumpatia Amata, naye akatupia jicho juu ya kioo na kuusoma ujumbe uliyoandikwa.

‘Usiku huu nitafanya msilolitegemea, free Somali Land’

Baada ya kuusoma ujumbe huo akatazama saa ngapi ulitumwa, akagundua kuwa haikupita hata saa tatu ni saa mbili na dakika kadhaa. Tofauti kati ya muda wa ajali na muda was ms ile ni dakika kama ishirini na nne hivi.

“Nini hiki?” akauliza huku akimpa Chiba simu ile.

“Utashangaa kwa kuwa hujui hili, huu si ujumbe wa kwanza ni wa tatu sasa, na namba ndiyo hii, ‘unknown’, Chiba pale anajua na imemtesa sana kuifuatilia,” Simbeye akasema. Amata akamtazama Chiba kana kwamba anamuuliza, ‘ni kweli?’

Namba zake zimefungwa kwa code ngumu sana, nimejaribu mara kadhaa lakini nimeshindwa kumpata mtumaji…”

“Na umeamua kuacha?” Amata akauliza.

“Si kuacha ninamsaka bado, nitamtia nguvuni tu, na asije kujaribu siku akapiga simu ndiyo utakuwa mwisho wake,” Chiba akazungumza kwa uchungu.

“Simbeye, mimi naweza kuichukua ajali hii kama hujuma katika sakati ambalo tunadili nalo kwa sasa, kwa mbali ninaanza kuona nini kinajiri, nakuhakikishi, huyu mpumbavu nitamleta hapa umle nyama,” akasema na tayari akawa wima kwa safari.

“Unaenda wapi?” Simbeye akamuuliza.

“Nataka niwe karibu na Madam S, ili akiamka tu anambie nini kimemsibu,” akajibu.

“Good! Hata mimi nipo kwenye kumtafuta juha huyu, nikipata fununu nitakwambieni, ila kwa sasa tuondokeni wote kwenda Muhimbili,” akawaambia kisha wote watatu wakatoka na kuingia garini. Safari ya kuelekea Muhimbili ikaanza, wakapita barabara ya Bibi Titi ili makusudi kufika eneo la tukio, wakati huu kulikuwa kimya hakuna mtu.

“Walizamilia kumuua,” Chiba akasema.

“Na hawatampata!” Chiba akajibu huku tayari wakiingia katika uwanja wa hospitali hiyo, haraka haraka wakateremka na kuliende jengo la wagonjwa mahututi. Wakiwa hatua chache kabla ya kulifikia lango kuu wakakutana na watu kama wane hivi waliokuwa wakizungumza kwa lugha ya Kifaransa, Amata akasimama na kuwatazama, kisha akamtazama Chiba.

“Vipi unawajua?” akamuuliza.

“Hapana, isipokuwa mmoja wao kama nimewahi kukutana naye vile,”

“Wapi?”

“Sikumbuki, ila nimewahi kukutana naye,” akajibu kisha wakaingia ndani na kumkuta Scoba na Gina wakiwa katika ulinzi madhubuti. Gina akaamka mara moja na kumuendea Amata.

“Vipi Kamanda… tetesi yoyote?”

“Hakuna kitu, mbingu bado nyeusi!”Amata akajibu huku akimshika mkono na kumvutia pembeni, kisha kwa sauti ndogo ya kuwatosha wao akamnong’oneza.

“Kuna watu wamekuja hapa kumwona mama?”

“Ndiyo wamekuja, lakini tumewakatalia kuingia, kwani hamjapishana na watu fulani hapo nje?”

“Ndiyo maana nimekuuliza…” Amata akamwambia. Wakati wao wakijifanya kuongea peke yao kumbe Inspekta Simbeye amewasiki vyema kabisa, na Amata alipachana na Gina na kurudi kuungana na wengine, Simbeye akamwambia.

“Ina maana we wale huwajui?”

“Hapana, ila mmoja nimeshawahi kukutana sehemu…”

“Wajumbe wa Baraza la Usalama la AU ambao wameweka kambi hapa Dar kwa ajili ya kuendesha oparesheni ile ya kumsaka muuaji shetani,” akamwambia.

Muda huo huo, Dkt. Jasmin akaungana nao, haraka, Simbeye na Amata wakamdaka juu kwa juu na kumvutia pembeni kwa mazungumzo.

“Vipi, mmegundua nini huko?” Amata akawa wa kwanza.

“Madam hajaumia yaani kupata majeraha, ila inaonekana amejipiga kichwani ndo maana amepoteza fahamu..”

“Ndani ya kichwa hakuna tatizo kubwa?” Simbeye akauliza.

“Hapana, hajapata tatizo lolote baya, na ataamka tu, tunaamini atakuwa na kumbukumbu zake sahihi kabisa,” Jasmine akawajibu na kila mtu moyo wake ukatua.





SEHEMU FULANI JIJINI DAR’

“Mmefanikiwa?” sauti nzito ya mwanaume aliyeshiba ikawauliza vijana wawili waliokuwa wameketi mkabala na mtu mzima huyo.

“Ndiyo, kwa kufuata maagizo yaleyale, tumefanya vilevile, na tunaamini kama hajafa pale basi atakufa kesho tu,” mmoja wa vijana wale akajibu.

“Safi sana, huyu mama, anaongoza kitengo nyeti sana cha usalama, na kitengo chake kina watu wasiojuliaka wasioshindwa kitu… lakini safari hii kapatikana, kwanza mmoja wa vijana wake aliyetikisa mpango huu ameuawa huko Sierra Leone, na hawatapata hata kucha yake…”

“Kazi ya Gupter hiyo!” akadakiza kijana mwingine.

“Aaaa yule mshenzi habahatishi… sasa ninyi mkapumzike kazi yenu mmeimaliza,” akaagana nao kisha yeye akabaki sebuleni hapo kwa dakika kadhaa kabla hajaondoka na kuliacha peke eneo hilo.



SIKU ILIYOFUATA

ADDIS ABBABA - ETHIOPIA

AMANDA KELLER aliwasili salama kabisa katika Jiji la Addis Abbaba tayari kwa kazi huku akiwa na taarifa nzuri kichwani ya kifo cha mwanamke mtata huko Tanzania. Akiendelea kupiga mruzi, akatoa sigara yake na kuiwasha kisha akaipachika kinywani. Kichwani mwake alijenga wazo moja tu, ni kutafuta ratiba ya wageni watakaokuja katika mkutano huo ilia aangalie njia zote ambazo atamtengeneze Martin Gupter kumaliza zoezi lake na kisha kukamata kitita cha pesa na kurudi nyumbani akiwa Bilionea na kuwaacha Waafirika wakiendelea kumalizana, ama hakika, wajinga ndo waliwao. Akiwa kabana sigara yake kinywani na begi dogo mkononi mwake akavuka barabara na kfika upande wa pili ambako alichukua usafiri kuelea mjini.

Katika hoteli ya kisasa ya Plaza, Amanda alijipatia chumba katika ghorofa ya sita, mara baada ya kukabidhiwa chumba akajibwaga kitandani na kumezwa na wimbi la fikra. Juu ya kitanda kikubwa aiweka karatasi kadhaa tayari kuanza mipango yake ya kujua ratiba na utaratibu mzima utakaotumika wakati wa mkutano huo. Moyoni mwake alijua wazi kuwa maadam yeye kapenya tayari ndani ya nchi hiyo basi isingekuwa ngumu kwa wengine nao kuingia yaani Fred na Martin. Akawasha TV ya taifa hilo na kuanza kufuatilia habari mmbali mbali kupitia idhaa ya lugha ya Kiingereza. Kupitia matangazo hayo alianza kupata mambo machache kuhusiana na ujio wa viongozi hao.

Naisubiri kesho! Akawaza wakati akiingia bafuni kujimwagia maji ili apate kupumzika na kujipanga kwa siku inayofuata.

* * *

Asubuhi ya siku iliyofuata, Amanda aliwasili katika ofisi za Umoja wa Nchi za Afrika zilizopo makao makuu. Hapo alijitambulisha kama mwandishi wa habari kutoka chombo kimojawapo huko barani Ulaya. Akaonesha vitambulisho na nyaraka nyingi nyeti za kumthibitisha kuwa ni yeye akiwa kajivika jina la kibandia Jennette Monsour. Baada ya maswala ya usalama kuzingatiwa, aliruhusiwa kuonana na mratibu wa mkutano huo ambaye alimpatia taarifa muhimu tu zinazomhusu yeye kama mwandishi ikiwamo muda wa kuwasili viongozi, hoteli watakazokaa na ratiba nyingine. Akamshukuru bwana huyo na kuaga.

Kila anakokwenda mwanamke huyu ilikuwa ni vigumu sana kumtambua kwani alikuwa na umbo na sura inayoweza kubadilika na kuwa mtu mwingine kabisa. Madawa na make-ups anazotumia zilitosha kumfanya mara Mchina, wakati mwingine Mmongolia, au hata Mmisri alishindwa tu kujiweka kuwa Msudani Kusini.

Amanda alitoka na moja kwa moja akarudi hotelini kwake na kuweka kila kitu sawasawa, kazi iliyobaki ni kutembelea hoteli hizo ili ajue ni jinsi gani zilizvyojengwa ikiwamo mipangilio ya vyumba ukumbi wa chakula na milango ya dharula. Hii ilikuwa ni lazima kufanya kabla ya shambulizi ili endapo ikibidi kutoroka kama hali imekuwa mbaya basi ujue ni wapi kwa kutokea. Hii ndiyo kazi kubwa ya mwanamke huyu, na ndiyo hasa aliyojifunza akiwa huko Israel na amewahi kuhusika kwenye operesheni tofauti tofauti na kufanikiwa katika kiwango cha juu.

Katika jokofu lililokuwa jirani na kitanda, akatoa pombe kali na kumimina katika bilauri, kisha akapiga yote tarumbeta na kuiweka bilauri hiyo mezani, kilichofuata ni kubadilisha nguo na kuvaa kisichana zaidi, akateremka na kuchukua usafiri binafsi yaani gari ya kukodi na kuanza kufanya ziara katika hoteli kubwa tatu ambazo viongozi hao wa juu walitakiwa kufikia.



DAR ES SALAAM

Kamati iliyoundwa ya Baraza la Usalama, ilivunja ofisi yake kwa muda na kuhamia Addis kwa sababu maalum. Siku hii walipokuwa wakivunja kamati hii, wapelelezi walilkuwa wametumwa kufanya chunguzi za awali juu ya mauaji ya viongozi walifika kwa nyakati tofauti kuleta taarifa zao. Taarifa ya kila mmoja ilileta majibu tofauti kidogo kuhusu ama muuaji au kikundi cha wauaji, ijapokuwa wote waligundua kuwa muuaji ni raia wa Kizungu lakini walishindwa kupata jina halisi na ni raia wan chi gani na anaishi wapi. Hatua ya pili katika hili ilikuwa ni kuweka taarifa pamoja ili kuchambua kipi chuya na kipi mchele.

Jina la Fadick Al-Habib lilijitokeza tena kutoka kwa mmoja wa wapelelezi hao ambao alikuwa upande wa Somalia ambako ndiko haswa kunakogombaniwa.

“Hapa naona wazi kuwa kuna mkanganyiko… hawa wengine wote hawajamgusa huyu Fadick lakini na huyu aliyemgusia hajang’amua kama kuna huyu mzungu, sasa which is which?” mwenyekiti akauliza jopo.

“Aaaah unajua mara nyingi muuaji kama huyu si rahisi kujionesha kwa sura moja… anaweza kuwa anajibadili sura na pia jina, hivyo sisi tuweke taarifa zote pamoja na tumtazame kama mtu anayejibadili sura na jina,” mjumbe mwingine akamjibu mwenyekiti wake na wengine wakatikisa vichwa kuwa wamekubaliana na hilo.

“Ok, sasa nafikiri hii operesheni iendelee katika mtindo kuwa huyu muuaji atafika Addis, hivyo nguvu kubwa ya hawa watatu na wengine tuiweke pale, hata sisi tunatakiwa tuwasili kule ndani ya saa ishirini na nne kutoka sasa,” Mwenyekiti akawaambia.

“Na hatujaandaa taarifa ya mjumbe mwenzetu Madam S ya kuhusu ajali…”

“Achana nayo, tuangalie ya msingi kwanza, maadam anapata matibabu basi haina shida, nitamwambia katibu afanye hiyo kazi wakati sisi hatupo,” Mwenyekiti wa kamati akamkatisha mjumbe na kisha akasimama.

“Tuonane Addis, lakini kila mtu atimize majukumu yake kabla ya kufika huko, mtasafirije; kila kitu kinaandaliwa,” akawaambia na kufunga kabrasha lake kisha akapotelea katika moja ya milango ya nyumba hiyo. Wajumbe hawa watatu nao kila mmoja akainuka kwa dakika yake na kuondoka, meza hiyo ikabaki nyeupe, hakuna mtu.

* * *

Mchana wa siku hiyo, Madam S alifumbua macho akamtazama Dkt. Jasmini, kisha wote wakatabasamu.

“Jasmin!” akaita kwa taabu kidogo na hakuweza kugeuza shingo yake kutokana na vitu vilivyofungwa shingoni mwake. Jasmin aliposogea karibu na kitanda, akanong’onezwa kitu.

“Mwite TSA 1 na 2 haraka,” akamwambia na ni dakika hiyo hiyo, msichana huyo akainua saa yake na kuibofya mahala fulani kisha akatuma ujumbe wa sauti ambao huko kwa wahusika ungesomeka kama nukushi kwa kupitia saa zao za mkononi. Dkt Jasmin akaendelea kumpa mazoezi madogo madogo mwanamke huyo kwa dakika kama kumi hivi.

“Unajisikiaje?” akamuuliza.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Uchovu, ila nina maumivu kiasi upande wa kushoto wa shingo,” akamjibu.

“Utapona tu!” Jasmine akampa matumaini huku akiweka mambo yake vyema kwenye kabrasha lililokuwa linaning’inia katika kitanda cha mama huyo. Akaondoa mashine ya kusoma mapigo ya moyo baada ya kuona yamerudi sawasawa, akamdunga sindano ya maumivu na kukiinua kitanda kiweka amekaa kwa nyuzi kadhaa.

“Asante binti!” Madam akamshukuru, “Fanya unachoweza, nahitaji kutoka,” akamwambia.

“Aaaaa mama bado inabidi uwe hapa kama siku tatu hivi!” Jasmini akamwambia.

“Ah no! hapa nahitaji kutoka, na unipeleke ama Shamba au hospitali ya jeshi ya Lugalo,” akatoa maagizo na mara mlango ukafunguliwa, Amata na Chiba wakaingia wakitweta.

“Madam S! aaaa Mungu mkubwa!” Amata akashukuru Mungu huku akikikaribia kitanda kile.

“Kumbe na we unaamini Mungu!”

“Usipoamini Mungu utamwamini nani katika dunia hii?” Amata akauliza.

“Sijui!” akamjibu, “TSA 1, TSA 2 naomba mulitafute gari namba TZC 452X,” akaongeza.

“La nini?” Chiba akauliza.

“Ndilo lililonigonga, na najua wanjau kuwa nimekufa”.

“Ulwahi kuona sura ambazo ziikuwamo ndani ya gari hilo?”

“Hapana, ila lilinigonga kwa makusudi kabisa, kama nisingetumia ujanja wa kujiokoa basi sasa imngekuwa mmeweka turubai Masaki,” akawaambi.

“Umesomeka Madam!”

“Sawa na pia mkinikosa hapa mjue ama Shamba au Lugalo!”

“Sawa! Kuna task nyingine ya kufika Sierra Leone kumuadabisha Martin Gupter,!” Amata akamwambia Madam.

“Sawa, mwambie Gina akufanyie mpango uondoke leo usiku, ila hakikisha unakuwa makini sana kuliko mwanzoni, jiepushe na wanawake,”

“Sawa mama!”

“Ila kabla hujaondoka, hakikisha umepata taarifa za hilo gari na uwaachie kazi wadogo zako … ok all the best!” Madam S akampa Baraka na rai kijana wake kisha wakaondoka zao na kumwacha hospitali hapo.

Ndani ya gari Amata akamwambia Chiba, “nilikwambia! Na nilijua tu kuwa kama ikitokea ameamka atatuambia kitu, haya sasa hii si ajali lakini je inahusiana na kabrasha letu?”

“Kabrasha gani?”

“Magnum 22,” akamjibu.

“Mtihani!” Chiba akajibu kwa mkato na kuwasha gari, akaondoka na kuiacha eneo hilo la Muhimbili kuelekea mjini. Breki ya kwanza ilikuwa ni katika ofisi za TRA Mtaa wa Samora ambako waliongoza mpaka kwa meneja na kumwambia kuwa wanahitajia kujua umiliki wa gari namba hiyo. Meneja yule akawapokea na kuwataka wafike katika kitengo cha usajili wa magari.

“Kwenye mtandao wetu gari iliyosajiriwa kwa namba hii ni Peugeot 405 new model, mali ya Blastus Chota!” wakajibiwa.

“Ok, tuprintie hiyo kadi ya gari,” Amata akamwambia na yule jamaa akafanya hivyo. Wakaagana na kuondoka zao.

“Mhm! Tunafanyaje sasa?” Amata akamuuliza Chiba.

“Kazi rahisi sana wala isikusumbue kichwa, twende TTCL tutapata mawasiliano yake na kujua wapi anapatikana,” Chiba akamweleza Amata wakati wakiingia kwenye maegesho ya ofisi hizo ambayo nayo yapo kwenye barabara hiyo hiyo. Hawakuhitaji kwenda mbali sana, mapokezi tu palitosha kumaliza shida yao baada ya kuonesha vitambulisho vyao. Kutoka hapo waliweza kujua ni wapi huyo bwana mwenye gari hiyo anapatikana.

“Yaani twende sasa, huyu lazima awekwe chini ya ulinzi sasa,” Chiba akamwambia Amata.

“No, tumpe kazi Inspekta apeleke CID wakafanye kazi hiyo, sisi tusubiri akiletwa kituoni,” Amata akashauri vinginevyo. Wakakubaliana na kutoka hapo wakaelekea kitu cha polisi cha kati ambako walikutana na mzee huyo na kumpa kazi.

“Hii? Mchana huu huu itakamilika,” Simbeye akawapa matumaini na hapo hapo akamwita kijana mmoja mkakamavu aliyevaa kiraia, akampa kazi na kumtaka animalize mapema iwezekanavyo.

“Mama anaendeleaje?” akawauliza.

“Ameamka, yupo ok!”

“Kweli? Naenda sasa hivi kumuona nina jambo la kuzungumza naye,” akawaambia huku akiinuka kitini na kwa kutumia simu yake ya upepo akaita gari ambalo daima hulitumia kwa shughuli zake, wakati mwingine huwa anaendesha ,wenyewe na wakati mwingine huwa anaendeshwa inategemeana na kazi anayokwenda kufanya.

* * *

Mchana wa saa nane, Kamanda Amata akapata taarifa kuwa Blastus Chota amepatikana na tayari amefikishwa katika kituo cha polisi cha kati. Bila kuchelewa, akaingia garini na kuelekea huko akiwa na Chiba. Haikuwachukua muda kufika kwani hata mahala walikuwapo hapakuwa mbali sana. Ndani ya chumba kidogo chenye viti viwili tu na kijimeza katikati alikuwa ameketi mtu huyo. Hakuwa mzee sana wala kijana sana, kutoka katika macho yake tu, Amata akaona kutokuwa na hatia kwake bali wasiwasi uliojaa pomoni.

“Mfungue pingu, huyu si mhalifu, nahitaji kuzungumza naye mswala machache tu kisha mtamrudisha,” akawaambia vijana wa polisi nao wakafanya hivyo kisha wakatoka na kumwacha mtu huyo akiwa na Amata na Chiba.

“Mr. Chota, utusamehe kwa hili, bali tulikuhitaji kwa mazungumzo machache kisha utarudishwa utokako, lakini hili litafanyika tu kama utatoa ushirikiano mzuri,” Amata akaanza mazungumzo.

“Sawa, sawa, hamna tabu, nitatoa ushirikiano wote, nitaeleza….” Chota akajibu kwa kitetemeshi.

“Sawa!” Amata akaitika na kumtazama Chiba. Chiba akachukua ile karatasi ya kivuli cha kadi ya gari, akaiweka mezani.

“Unaitambua kadi hii?” akamuuliza.

Blastus Chota akaitazama kwa sekunde kadhaa na kumwangalia Chiba, akatikisa kichwa juu chini kisha yakafuatia maeneno, “ndiyo, naitambua, hii ni gari yangu!”

“Gari yako?”

“Ndiyo, ni gari yangu lakini kwa sasa imekwishaibwa!”

“Imeibwa! Unaweza kutuambia lini imeibwa?”

“Ina mwaka karibu na nusu sasa, ni Peugeot moja ya gharama sana, nilinunua Ufaransa mwaka 1999,” akawajibu.

“Uliripoti polisi?”

“Ndiyo! Niliripoti kituo cha Usalama Magomeni, baada ya mwezi nikaambiwa kuwa imeonekana gari yenye namba kama hizo lakini si Peugeot ni Land Rover Defender, wakati huo ndo zilikuwa zikiingia nchini, basi, baada ya hapo hakuna kilichoendelea, nikapigwa danadana mpaka nikaamua kuacha,” Blastus akajibu na kunyamaza kimya.

“Unamkumbuka askari aliyekuwa na kesi hiyo?” Chiba akazidi kuchimba.

“Namkumbuka sana tu, anaitwa Jafari Kibanga alikuwa kitengo cha upelelezi yaani CID,” akaeleza.

Chiba akaandika vitu fulani katika kijiratasi kidogo kisha akamwita Amata kando na kuongea naye maneno machache, baadaye wakamwita askari mmoja na kuzungumza naye. Baada ya dakika kama kumi hivi wakaondoka na gari binafsi, Chiba, Amata, Blastus na yule askari. Safari yao ikaishia kituo cha polisi cha Oysterbay, baada ya kujitambulisha na kusema shida yao, mkuu wa kituo hicho akamwita kijana wake Jafari Kibanga. Askari huyo aiyekuwa amevalia kiraia alishituka sana kukutana macho kwa macho na Bwana Blastus Chota. Akaketi kitini kama alivyotakiwa huku akiobekana wazi kuvhanganyikiwa kwa mbali.

“Afande Kibanga, hawa mabwana wanatoka kituo cha polisi cha kati, wamekuja kukutafuta wewe, sasa naomba uwasikilize shida yao,” mkuu wake akamwambia.

“Sawa afande!” Kibanga akajibu.

“Afande Kibanga, unamtambua mtu huyu?” Chiba akamuuliza.

“Ndiyo namtambua…”

“Kwa vipi?”

“Huyu bwana kwanza anaitwa Bwana Chota…”

“Haswaa….”

“Huyu bwana aliibiwa gari, Peugeot, na mimi ndiye nilipewa jukumu la kufuatilia ile kesi yaani kushirikiana na watu wa usalama barabarani kujua ni wapi gari lile limepotelea…”

“Enhee! Sasa tuambie mlifanikiwa kulipata au la?” Chiba akazidi kupiga maswali.

“Hatukuliona lile Peugeot, ila kuna kipindi tulikamata LandRover yenye namba hizo…” Kibanga akauliza.

“Sawa, baada ya hapo mkafanya nini?” Chiba akauliza.

Kibanga akabakia kimya akimwewesa midomo yake, akakosa jibu la kuwapa, mapigo ya moyo wake yakawa yakienda kasi bila mpangilio.

“Tulimpata mmiliki wa gari lile… aaaaahhnn tukamueleza kuwa tunataka gari halisi lenye namba hizo, aaaa tukaambiwa tusubiri, baada ya siku tatu ambazo nilimwambia huyu bwana aje kituoni, asubuhi yake tukakuta ujumbe kutoka kwa Mkuu wetu bwana Matinya, kuwa tuliache hilo gari liondoke, na tusifuatilie tena hiyo kesi, nilitaka kujua kwa nini, nikaitwa ofisini nikaambiwa niachane na swala hilo, lakini katika udodosi wangu nikagundua kuwa lile Defender jipya kabisa ni mali ya Mheshimiwa Balozi Bailhani,” Kibanga akaeleza.

“Kwa hiyo ina maana Balozi Bailhani alihusika na wizi wa gari la huyu jamaa?”

“Inawezekana!”

“Asante sana kwa ushirikiano wako naomba turudi ofisini!” Chiba akasema na wote wakaagana kwa kupeana mikono Amata na timu yake wakaingia garini na kuondoka.

“Sasa, ina maana nitalipata gari langu?” Blastus akauliza.

“Litakuwa limeshabomoka, bado ybalihitaji tu?” Amata akamtania.

“Aaaaaa my favourite car, hata nikipata mlango tu mi nauchukua,” akajibu na wote wakaangua kicheko.

“Ok sasa tutakurudisha walipokuchukua, kama kuna lolote utapigiwa simu, ila kwa sasa tulia kimya na usiseme habari hii kwa mtu yeyote,” Chiba akamwambia wakati gari likiingia katika maegesho.

“Asanteni sana!” Bwana Chota akawashukuru nao wakaingia garini na kuondoka mpaka kituoni cha kati.

“Sasa afande, kuhusu hili tumemaliza, kama tutahitaji msaada wako tutakutafuta,” Amata akamwambia yule kijana wakaagana na kuondoka zao.

* * *

Mara baada ya kuachana na yule afande, Chiba na Amata waliongoza kwenda ofisi ndogo kwa ajili ya kuweka mambo mengine sawa. Siku hii hakukuwa na mtu ndani ya ofsisi hii kwani mwenye nayo alikuwa hospitalini baada ya kupata ajali.

Sina imani na kamati ndogo ya Baraza la Usalama!

Maneno haya yalikuwa yameandikwa katika kikaratasi kidogo kilichoachwa juu ya meza kana kwamba mwandishi wake alikuwa amekwishakisahau, lakini haikuwa hivyo, bali aliyekiacha alikusudia, lakini alifanya hivyo kwa madhumuni gani?

Kamanda Amata akakichukua na kukisoma mara nyingine kwa ukaribu sana, kisha akakitua kwenye chano ndogo yenye vijikaratasi vingivingi.

“Vipi?” Chiba akauliza.

“Aaah vijikaratasi vya bi’ mkubwa hivi!” akamjibu huku akijituliza vyema kitini.

“TSA 2, sasa namwona Mkuu wa Itifaki kwenye dishi langu…” Amata akamwambia Chiba.

“Kivipi?”

“Gari lililomgonga Madam S ndilo lenye namba hizi, na hizi namba ni bandia kwani gari halisi la ni hilo Pijo la Bwana Chota. Na katika maelezo ni kwamba gari hii ya Defender iligundulika kuwa na namba hizi, na Defender hiyo ni mali ya Balhani… kuna nini hapo?” Amata akafafanua.

“Mh! Atakuwemo, how?”

“Siku nilipokwenda Kunduchi, niliambiwa kati ya wateja wa mwanamke yule mshumami, Bwana Bailhani yupo, na huwa anaenda mara nyingi tu kumwona na kutafuna naye maisha…” Amata akamwambia Chiba.

“Je Bailhani atakuwa ndani ya mpango?”

“Probably! Madam S alinidokeza kitu, siku ya mkutano ule wa AU hapa nchini tulipoamua kuusitisha kwa saa kadhaa yeye alibisha sana na nasikia hata alidiriki kumtishia mama kuhusu hilo. Sasa tujumlishe…”

“Bailhani huyu mkuu wa itifaki?”

“Haswaaaa!!! Hakuna mwingine… inawezekana kwa asilimia hamsini na moja kuwa ndiye aliyeisababisha ajali hii, yaani anahusika,” Amata akasema.

Amata na Chiba wakazungumza mengi kuhusu sakata hilo na kuweka mambo sawa tayari kwa kazi.

“Sasa mi naondoka usiku huu, cha kufanya msimguse Bailhani, mwacheni awe huru, nikimaliza kazi Sierra Leone nitawapa taarifa ya kumtia mbaroni, lakini kaa tayari muda wowote naweza kukuhitaji katika uwanja wa mapambano,” Amata akamwambia Chiba.

“Usiwe na shaka kaka, For my people, For my nation!” Chiba akamjibu mkubwa wake kwa cheo.

“Nakwambia ukweli, timu teule ya AU katika upelelezi huu wa kazi hii sijui kama wataweza kirahisi… hawa jamaa wana mtandao, na nimeugundua, kuanzia Angola, Tanzania, Emirates na ni nina uhakika ndani ya AU yenyewe,” akamwambia Chiba.

“Ni kweli…”

“Sasa tukutane kwa Madam S, nitakwenda kumuaga jioni hii, kwa sasa naelekea nyumbani kujiandaa,”

“Sawa Kamanda, najua ni jinsi ganii upo tayari kuliokoa taifa na Afrika dhidi ya watu wasioitakia mema. Tuko pamoja, pale tu utakapoona unahitajia msaada wa haraka, nipe taarifa na uingie mafichoni mpaka nitakapofika, tutawaweza tu, na tutapigana mpaka mwisho wa uhai wetu…” Chiba akazungumza na kumpa mkono Amata, mkono wa heri na Baraka kwa safari yeke ya kufa na kupona.







FREETOWN

ALFAJIRI YA SAA kumi na moja, Kamanda Amata aliwasili katika jiji la Freetown, alifurahia zaidi kufika muda huu kwa sababu maalum, kwanza alikuwa na uhakika kuwa hakuna mtu mbaya anayemuona na pia alijua wazi kuwa kama mambo yatakwenda vizuri basi siku hiyohiyo angeweza kufika anakokutaka. Katika kijitabu cha kumbukumbu alichpewa na marehemu Inocent kule katika kaburi la halaiki kulikuwa na ramani ya kufika mpaka katika jumba linalokusudiwa kuwa Martin Guter na timu yake hujificha kila baada ya uhalifu.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Nje ya uwanja huo akachukua gari la kukodi na kumtaka dereva kumfikisha katika hoteli ile ile aliyofikia mwanzo, hoteli ya Swizz Spirit. Katika meza ya mapokezi akapokelewa bila tatizo lolote na kupatiwa chumba anachostahili. Ndani ya chumba chake hicho, Amata alijikuta anashikwa na hasira ghafla akiwa ndani ya chumba hicho, akamkumbuka mwanamke ambaye alimhadaa kimapenzi na kumtumbukiza kwenye hatari kubwa.

“Naanza na yeye!” akajisemea huku akiuweka mkanda wa suruali yake kitandani nay eye kuingia maliwato. Baada ya kuoga na kujipulizia manukato akajitupa kitandani japo apate usingizi wa saa mbili au tatu hivi.

* * *

Majira ya saa nne asubuhi, Amata akatoka ndani ya hoteli hiyo akapita mlango wa nyuma na kujikuta kwenye maegesho ya magari, hapo akachukua taksi na kuelekea nyumbani kwa yule mwanamke. Hakuwa amesahau njia, alimwongoza yule dereva mpaka mbele kabisa ya ile nyumba. Nyumba hii ndogo lakini ya kisasa ilikuwa imejitenga na nyingine, ilikuwa imezungukwa na maua mengi na miti kadhaa ya kuifanya iwe kivulini. Akamlipa dereva taksi na kumtazama akiondoka kutoka katika uwanja wa nyumba hiyo, kisha akaigeukia na kuutazama mlango mkubwa. Nje ya nyumba hiyo kulikuwa na gari moja la kisasa sana, Aston Martin.

Bila shaka kuna kibopa anayejifaidia! Akawaza na kujiweka tayari kuikabili nyumba hiyo, akazikwea ngazi na kuufikia mlango, akachukua funguo yake na kuipachika tunduni, hakupata shida; mzunguko wa kwanza, wa pili, kitasa kimeachia, akajitoma ndani. Sebule ileile ikamkaribisha, akatazama mandhari yake, haikuwa imebadilishwa, jicho lake likaugonga mlango wa chumbani. Akauendea na kuuskuma taratibu, naam, hakukosea, aliyemtaka alikuwa kajilaza kitandani kama embe dodo, akiwa hana hata kipande cha nguo maungoni mwake. Maji yaliyokuwa yakitiririka yalisikika kutoka mlango wa bafuni. Akapiga hatua nyingine kadhaa na kukifikia kitanda hicho huku tayari mkononi bastola ‘Berreta’ ikiwa tayari.

“Nimekupata!” akasema, na kumfanya mwanamke yule kushtuka, Amata akazunguka kitanda mpa upande wa miguu na kusimama akimtazama mwanamke huyo akijikusanya na kujisitiri kwa shuka.

“You have died!!!” akapiga kelele akimaanisha kuwa mtu huyo alishakufa.

“Yes! I have died and now, I have risen!!!” Amata akamwambia. Akiwa katika hali hiyo hisia zake zikampa taarifa kuwa mlango wa bafuni unafunguliwa, akageuka haraka na kutazama.

“Tulia! Njoo uungane na mkeo hapa!” akamwambia kwa Kifaransa safi kisichoghoshiwa.

“Lakini si-si-na hatia…” akajitetea mwanamke huyo mwenye asili ya kihindi. Kwa macho ya haraka haraka, alionekana wazi kuwa na umri mdogo kuliko hata mwanamke aliyelala naye.

“Ndiyo, hauna hatia, ila tu hujui kuwa umelala na jambazi, ambalo linalaghai wanaume na kisha kuita watu wake wakuue…” Amata akasema. Yule kijana akamtazama mwanamke wake na kumtolea macho.

“Unaona hajibu? Anajua kazi yake…”

“Mimi si jambaziiiii!!!!” yule mwanamke akasema kwa sauti.

“Kimya!” Amata akamkemea huku akiwa kakunja sura isiyo na chembe ya huruma, “Nataka unipeleke mguu kwa mguu kwa wale majambazi wako,” akamwambia.

“Sipajui wanapoishi na wala siwajui watu wale….” Kajibu huku akibubujikwa na mchozi.

“Hupajui kivipi? Wakati wewe ndiwe uliyewaita waniue, ulifikiri huwa nakufa kirahisi? Basi sikufa na sasa nimekuja kwa ajili yenu washenzi nyinyi!”

“Mimi siwajui….”

“Haya nambie ilikuwaje wakanikuta hapa kama si mbinu zako….” Amata akamtaka mwanamke huyo kumpa habari yote. Yule mwanamke akaeleza kila kitu kuanzia A mpaka Z.

“Kwa hiyo ulinisaliti kama Yuda alivyomsaliti Yesu, ukaniwekea na ua waridi kitandani, ukinidanganya kuwa wekundu wa ua lile ni rangi ya upendo kumbe ni damu itakayomwagika, dah!”

“Sammaahhaanni sana!” yule mwanamke akaomba msamaha na kushuka kitandani akiwa uchi, akapiga magoti na kuishika miguu ya Amata akilia. Kamanda si kwamba alikuwa akisikiliza sauti hiyo ya kuomba msamaha bali umbo malidhawa la mwanamke huyo, lenye utamu wa kila namna na wenye kumpendeza kila mwanaume rijali, mwii ambao haujakobolewa, upon a uasili wake wa kutoka tumboni mwa mamaye. Akajikuta anameza mate hata kama hakutaka.

“Sasa, mguu huu mimi na wewe mpaka walipo, kwa kuwa wewe ulishuhudia kifo changu sasa nataka ukashuhudie vifo vyao…” Amata akamwambia huku akiiweka bastola yake kiunoni.

“Nipo tayari,” akaitikia mwanamke yule kisha akasimama na kuliendea kabati, akachukua suruali yake ya jinzi la kuvutika na kujitwalia, fulana kisha raba nyepesi, akachukua na kiburungutu cha pesa, akakisunda kwenye sidiria. Dakika kumi, akawa tayari kwa safari hiyo ambayo hata hakuijua ni wapi anapelekwa.

“Hey!” akamshtua yule kijana, akamtazama, “Lete funguo ya gari, ukae hapa ole wako uondoke na ole wako umwambie mtu kuhusu haya… nikukute hapa baada ya saa kadhaa, lala jifunike, mkeo atarudi uendelee kumndondomola,” akamliza kusema na kijana huyo akaiendea suruali yake na kuto funguo, akampatia Amata pasi na kunena lolote.

Amata na yule mwanamke wakaingia garini, hakika lilikuwa gari la kisasa sana, tangu aanze kuendesha magari hakuwahi kukaa kwenye gari la starehe kama hili, zaidi ni kuliona kwenye filamu za 007.

* * *

Hali ya hewa ilikuwa baridi na mvua za hapa na pale zikiendelea kunyesha, Kamandal Almata aliendelea kuendesha gari lile kwa kasi huku akiwa anaambaa sambamba na Mto Lofa. Simu yake iliyokuwa akimwongoza kwa kutumia mfumo wa GPS. Akaambaaambaa na barabara hiyo na kuanza kupanda milima mikali.

‘SILENT ROCK VILLA’ maandishi katika kibao yakamkaribisha, kichwani mwake akalikumbuka jina hilo kutoka kwenye kijitabu cha kumbukumbu cha Innocent ila kwa wakati ule hakuyaelewa kutokana na kwamba hayakuwa pamoja n ale ramani.

“Sasa huku tunaenda wapi?” akauliza abiria wake.

“We tulia si nimekwambia utashuhudia rafiki zako wanavyokufa!”

“Mh!” akaguna wakati Amata akiegesha gari juu kabisa ya kilima cha piali ambapo aliiona ile nyumba vizuri kabisa. Akatazama saa yake, saa saba mchana, akashuka na kusimama nje, baridi ilikuwa kali na yule mwanamke akamfuata na kusimama kando.

“Tunatakiwa twende pale,” akamwambia yule mwanamke ambaye mpaka dakika hii hakumjua jina lake.



Nimewahi sana! Muda mzuri ni jioni, no! sasa hivi…! Akajisemea moyoni na kuchukua kama sekunde kumi au kumi natano hivi kushirikisha mwili wake.

Naenda! Akakamilisha maamuzi na kuingia garini na yule mwanmke naye akaingia, Amata akawasha gari na kuigeuza, akaanza kuteremka mlima ule alioupanda mwanzo.

“Uwe tayari ni wakati wa mapigano makali, ama wao washinde au sisi tushinde,” akamwambia huku akibadilisha gia na kuteremka kwa kasi. Haikuwachukua muda mrefu, wakawa karibu sana na jumba lile, Amata akapinda kulia na kuingiza gari vichakani akalizima.

“Vipi, Mbona porini?” akaulizwa.

“Ndiyo tunaegesha gari hapa kisha tunakwenda ndani ya hilo jumba, au we unabaki?” Amata akamjibu.

“Nani abaki! We si umesema unataka nishuhudie hao jamaa wanavyokufa, twende wote,” yule mwanamke akajibu wakati Amata akikata baadhi ya matawi ya miti na kulundika kulificha lile gari. Dakika kumi na tano baadae, tayari akafanikiwa kulifanya lisionekane. Yeye na huyo mwanamke wakaanza kutembea taratibu kupita pori kwa poori kulielekea jumba hilo. Baada ya hatua chache wakakutana na ukuta mkubwa kama wa gereza, akautazama kuanzia juu mpaka chini. Akampa ishara mwanamke huyo na kuanza kutembea kuufuata ukuta huo mpaka walipokaribia lango kuu. Akampa ishara ya kusimama naye akafanya ivyo.

“Kaa nyuma yangu daima, usitoke!” Amata akamwambia kwa kunong’ona. Akatoa bastol kiunoni mwake na kuiweka tayari kwa kazi, magazine aliyoipachika haikuwa na risasi za moto, basi vitu kama vijishale vidogo vyenye urefu kadiri ya inchi moja ambavyo vina dawa ya usingizi inayoweza kukulaza kwa takribani saa tatu. Hatua nyingine kama kumi hivi zikamfikisha katika lango la kuiingia ngome hiyo, mbele yake kulikuwa na round about kubwa iliyojawa maua kedekede. Kwa jicho la haraka hakuona kamera yoyote ya usalama. Akajitokeza tayari kuuvamia mlango ule mkubwa wenye nakshi za kuvuti na kupambwa na maandishi yaleyale kama aliyoyaona kule kwenye njia panda. Aliapoanza tu kuuendea akasikia muungurumo wa gari ukitokea barabara kuu, akarudi nyuma na kuchuchumaa kwenye maua marefu, na yule mwanadada akafanya vivyo hivyo.

Sekunde thelathini gari moja jeusi likawasili ndani yake kulikuwa na jamaa Mwafrika akilindesha, lile lango likafunguka na taratibu. Amata hakutaka kuipoteza nafasi hiyo, kutoka alipokuwa yeye na ule mlango ni kama mita kumi hivi, akapiga hesabu ya haraka haraka ni jinsi gani anaweza kuingia pamoja na gari lile, akapata jibu. Kwa haraka akainguka na kuvuta hatua kwa kukimbia mpaka katika mlango wa lile gari, akau8fungua na kuketi kiti cha abiria huku tayari bastola ikiwa mbavuni mwa dereva. Yule mwanamke naye akafungua mlango wa nyuma na kuketi.

“Lala chini!” Amata akamwambia mwanamke huyo kisha akamwamuru dereva aendeshe kuingia ndani naye taratibu akaendesha na kuvuka lango hilo. Kama alitegemea kujikuta kwenye uwa au maegesho ya magari basi alikosea sana, gari lile liliingia katika sebule kubwa ya kupitab taratibu mapa katika moja ya kuta nayo ikafunguka kwa kwenda juu, likaingiamo. Mbele kidogo likasimama na yule dereva akamtazama Amata kwa woga.

“Unataka nini?” akamuuliza.

“Martin Gupter?” Amata akajibu.

“Gupter?” yule dereva akauliza

“Ndiyo…”

“Mbona simfahamu!” akashangaa.

“Humfahamu au unataka nitumie nguvu ndio unambie ukweli?” Amata akamwambia huku tayari keshamkunja shati lake. Yule dereva akaanza kutetemeka kwa woga.

“Hamkuwa na wageni wowote ndani ya jumba hili?” akamtupia swali kwa kuligeuza, “Wazungu watatu, mmoja mwanamke na wawili wanaume…” akaongeza kusema.

“Kulikuwa na watatu kama usemavyo, mmoja alikwishaondoka na wawili ndo sasa nimetoka kuwapeleka Uwanja wa Ndege,” akamwambia Amata.

“Wanakwenda wapi?”

“Aaaa mi sijui na wala sitakiwi kujua mimi hapa ni dereva tu, na wageni wa mzee sitakiwi kuwahoji chochote!”

Kamanda Amata akafyatua bastola na kile kishale kikamdunga jamaa shingoni, sekunde kumi tu akaanza kukodoa macho kama fundi saa anayetafuta skurubu. Amata akashuka na kufuatiwa na yule mwanamke, akapita katika uwazi mwingine na kujikuta katika ukumbi mkubwa ambao katikati kuna bwawa kubwa la kuogelea. Akalizunguka mpaka upande wa pili, akakwea ngazi na kufika ghorofa ya kwanza. Muda wote huu hakukutana na upinzani wowote, hapa akakutana na mlango mkubwa wa mbao, akakitazama kitasa na kugundua kuwa anaweza kucheza nacho, akachukua funguo yake na kuitumbukiza.

‘Twiiip! Twiiip! Twiiip! Twiiip!’ kelele kali za hatari zikasikika, Amata akajua amebugi, amefanya makosa, hakuna jinsi ya kuyasahihisha. Akamvuta yule mwanadada na kuingia naye kwenye uwazi mmoja ambao ndani yake kulikuwa na mtungi mkubwa wa maua, wakajificha nyuma yake na kusubiri. Mara watu wawili wakawasili, mmoja wao akachukua funguo yake na kuitumbukiza katika tundu, ile kengele ya hatari haikulia tena. Mambo yote haya amata alikuwa akiyashuhudia kwa macho yake.

Kumbe kuna funguo maalum! Akawaza. Alipowaona jamaa hao wanatoka, akajitokeza haraka na kuruka hewani, miguu yake ikatawanyika na kumtandika mmoja ambaye alisukumwa na kujikuta kingo za sakafu zikishindwa kumhimili, hivyo akadondoka vibaya na kutumbukia katika bwawa. Huyu mwingine alijibamiza ukutani akarudi wima na kukutana na kishale cha Amata, naye hakuchukua hata dakika akabebwa na usingizi.

“Chukua funguo!” Amata akamwambia yule mwanadada, naye kwa haraka akachukua, Amata akatazama huku na kule, hakuna shida. Akachukua funguo ule na kuingia ndani ya sebule kubwa, nzuri yenye samani za thamani. Amata akajikuta akitazama huku na huko, hata hakujua ni wapi ashike. Kando kabisa ya sebule hiyo kulikuwa na dirisha kubwa na meza ndogo ya kusomea iliyobeba kabrasha moja tu tena lilionekana kana kwamba limesahaulika, akaliendea huku nyuma yake akifuatwa na yule mwanamke, akalichukua na kulitazama, akasoma mawili matatu, moyo ukaanza kumwenda mbio, akaitazama saa yake.

“Shiiiittt!!!” akang’aka na kuikunja ile karatasi akaitia mfukoni na kuanza kurudi alikotoka. Akiwa anataka kumshika mkono yule mwanamke ili watoke kwenye jumba hilo, akasikia ‘clack’, milango yote ya kutokea nje ikajifunga. Akamwacha mwanamke huyo na kushika kitasa cha kwanza, umefungwa! Akauacha na kuuendea ule wa pili nao umefungwa, kengele za hatari zikagonga kichwani mwake.

“Tumeingia mtegoni,” akamwambia mwanamke huyo aliyekuwa naye.

“Sasa tunafanyaje?”

“Hatuna cha kufanya!”

Ukimya wa sekunde kadhaa ukatawala kati ya wawili hao, yule mwanamke akamsogelea Amata na kumkumbatia huku machozi yakimtoka.

“Kwa hiyo tunakufa?” akauliza.

“Hapana, ukiwa na mimi amini tu kuwa kifo kinaletwa na Mungu na si mwanadamu,” Amata akajibu huku akiliendea dirisha kubwa, akasimama na kuvuta kioo upande, macho yake yakashuhudia kolongo kubwa sana ambalo chini yake kuna mto Lofa uliyofanya mazingira ya kupendeza. Mara akasikia mlango ukifanya ukulele kuwa kuna mtu anafungua.

“Wanakuja!” yule mwanamke akasema.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Tulia,” akamjibu na kutzama huku na huko kuona jinsi ya kujiokoa, hakuna. Haraka sana, akasukuma kochi na kuuziba mlango ili angalau kuongeza kizingiti kwa watu hao. Amata akaingia chumba kingine na kugundua kuwa ni jiko, hapo akakuta kuna bomba mtepeto ‘hose pipe’, kwa ngumi moja akavunja kioo na kuchukua ule mpira wenye urefu kadiri ya mita hamsini hivi. Aliporudi katika ile sebule tayari jamaa walikwishafungua mlango.

“Kill him!!!!” mmoja alisikika akipiga kelele na mara Kamanda Amata akasikia milio kadhaa ya risasi, akajua zimemkosa. Kwa kasi akawahi lile dirisha na kumkuta yule mwanamke akihaha, akamdaka na kumzungushia mkono wake kiunoni.

“Hold tight!!!” Amata akamwambia mwanamke huyo naye akafanya alivyotakiwa. Amata akachukua bastola ya upande wa pili, yenye risasi za moto. Risasi ya kwanza ikamteremsha kiongozi wao, ya pili ikamvunja mguu mwingine. Amata akiwa kakamata ule mpira kwa mkono mmoja na mwingine bastola huku kabanwa sawia, akatumia nguvu zote na kujirusha katika dirisha, kioo kikatawanyika naye akajirusha nje.

* * *

“Hii ndiyo misheni ya mwisho!” Gupter akamwambia Fredy.

“Na inabidi tuipange kwa umakini wa hali ya juu maana najua kuwa usalama wte wa Afrika utakuwa hapo,” Fredy akamwambia Martin huku akiendelea kunywa mvinyo wake taratibu.

“Kwa uzoefu wangu, kwanza mpaka sasa watakuwa wamebana uwanja wa ndege, na mahotelini pia…”

“Lakini kwa mpango huu wa kushuka hawatatukamata hata kidogo,”

“Yeah!”

Martin Gupter na Fredy walikuwa wakibadilishana mawazo ndani ya ndege wakiwa hewani kuelekea Addis Ababa. Kazi iliyokuwa ikiwasubiri katika jiji hilo ilikuwa ya kufa na kupona lakini walijiamini kutokana na weledi wa kazi yao.

“Hatujawahi kushindwa!” Martin akamwambia Fredy.

“Tutaingia pale usiku lakini mpango wetu ni kama tulivyopanga, Amanda anatusubiri kadiri ya maelekezo tuliyompatia…” Martin akasema.

“Yaani mimi kwa kumdhibiti yule mshenzi wa Tanzania, tumefanya kazi kubwa, hawa wengine takataka tu,” Fredy akasema. Martin akabadili kutoka kutazama muvi kwenye sikirini mbele ya kiti chake na kuweka ramani kutazama ni wapi wapo.

“Tumekaribia, sasa tunafika ukingoni mwa Jangwa la Sahara, dakika kama kumi na tano hivi tutakuwa tumeianza Addis,” Gupter akamwambia Fredy. Freddy akanyanyuka kitini na kuvuta pazia kisha akafuata ujia wa kuelekea chooni. Ndani ya choo hicho alitulia kwa dakika kadhaa, si kwamba alikuwa akijisaidia bali ni moja ya mbinu ambayo walipanga na swahiba wake. Freddy na Martin waling’amua mbinu ambazo dhahiri shahiri zingeweza kutumika na wana usalama kuwanasa. Kati ya hizo ni kuweka makachero katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Bole. Kwa kugundua hivyo wakajipanga kutumia mbinu mbadala kuingia katika jiji hilo.

‘Ngoh! Ngoh! Ngoh!’ Freddy alisikia mlango ukigongwa mara tatu, akaufungua na kutoka chooni.

“Hili ni kwa ajili yako,” Martin akampatia Freddy parachute naye akalivaa. Wakiwa katika harakati hizo, mtumishi wa ndege hiyo akawakuta.

“Hey! What are you doing?” akawauliza wanafanya nini. Martin hakumjibu bali akachomoa kisu kutoka kwenye mguu wake ndani suruali.

“Be silence!” akamuonya kuwa kimya.

“Hatutaki kudhuru mtu ndani ya chombo hiki, sisi tuna kazi zetu na sasa tunataka kuondoka, tuoneshe njia ya siri kuingia katika chumba cha mizigo haraka,” wakamwamuru na huyo dada hakuwa na jinsi akawapitisha katika njia zao wambazo huzitumia kwa kazi zao huku wengine nao wakitahadharishwa kutofanya lolote. Baada ya sekunde chache, yule mwanadada akawaonesha njia ya siri kabisa inayoshuka chini ambako uhifadhiwa mizigo ya wasafiri.

“Please, don’t hijack a plane!” tafadhali msiiteke ndege! Yule mhudumu akawasihi.

“That is not our mission,” hiyo si kazi yetu! Martin akajibu huku akiufunga ule mlango na wao kupotelea chini. Huko wakapenyepenye mpaka usawa wa magurudumu ya nyuma, kwa kutumia vifaa vyao vya siri wakafungua kijimlango ambacho kiliwaruhusu kuona nuru ya nje. Upepo mkali ulianza kuingia ndani na kuleta vurugu. Kengele za hatari zikaanza kufanya fujo ndani ya chumba cha rubani, wakang’amua kuwa kuna hitilafu katika sehemu ya chini ya ndege. Mmoja wao akatumia njia maalumu ndani ya chumba hicho na kuingia katika sehemu ya mizigo, akapita kwa taabu kutokana upepo mkali akafika eneo husika na kutumia nguvu nyingi kudhibiti kijimlango hicho, akafanikiwa japo si kwa kiwango kikubwa. Dakika ishirini na tano baadaye ndege ile kubwa ikafanikiwa kutua salama katika uwanja huo na abiria waliokuwamo wakapiga makofi kumpongeza rubani kwa kuwa amewanusuru maisha yao.

* * *

VILIMA VYA ETONTO – ADDIS ABABA

Amanda Keller aliegesha garile katikati ya msitu Etonto ulio nje kidogo ya jiji hilo maarufu Afrika. Jua tayari lilikuwa likiimaliza safari yake ya siku nzima upande wa Maghalibi wa jiji hilo na kuanza kuliacha giza litawale. Sauti za ndege wazuri zilisikika pia zikiimba na wakirudi makundimakundi kwenye viota vyao ndani ya msitu huu. Akaitazama saa yake, ikamwonesha ni saa kumi na mbili na robo jioni; mara tu baada ya kuushusha mkono wake akasikia muungurumo wa ndege-Ulaya na kuiona ikikatiza anga kuelekea Bole ambako ndiko uliko uwanja mkubwa wa ndege wan chi hiyo. Akafungua mlango na kutoka nje ya gari hilo aina ya Jeep Cherokee. Haikupita hata dakika tano akasikia vishindo nyuma yake, akageuka na kutazama, akaona vitambaa vikubwa vikifunika eneo dogo lenye mzingo wa kama mita nane hivi na miguno ya watu ikasikika. Akakimbia mara moja na kuwasaidia japo kusimama.

“Natumai mmetua salama!” akawaambia.

“Yes, na sasa ni kazi moja tu! Vipi huko Addis, mambo yakoje?” Martin akauliza wakati Fredy akikunja ile miamvuli waliyotumia.

“Addis ni moto, ulinzi kila mahala, kila hoteli, kila baa na kila kilabu cha usiku, patroo za askari mchana na usiku…” Amanda akajbu huku akifungua mlango wa gari tayari kwa safari.

“Bila shaka wanataraji uwepo wetu,”

“Haswaaa, uwanja wa ndege wana usalama wengi wana picha zetu, wanategemea tungeingia kizembe sana ili watunase…” akaeleza.

“Wameula wa chuya kwa uvivu wa kuchagua,” Fredy akasema huku akifunga mkanda na gari lile likaondoka kwa kasi kurudi mjini.

Dakika hamsini na tatu ziliwafikisha katikati ya jiji hilo baada ya kupita vikwazo vingi vya askari na ukaguzi wa hapa na pale lakini hakuna askari hata mmoja aliyewagundua watu hao kutokana na jinsi walivyojibadili hapa na pale. Amanda akaendesha gari mpaka upande wa pili wa jiji hilo huko viungani na kuingia katika nyumba moja ya ukubwa wa wastani iliyozungukwa na miti mkubwa ya maua ya bugamvili na kufanya picha ya kupendeza.

“Makazi yenu yatakuwa hapa!” Amanda akawaambia baada ya kuegesha gari lake mbele ya nyumba hiyo. Wakateremsha mabegi na kuingiza ndani kila mmoja akachukua chumba alichokipenda.

“Hapa ni salama?” Martin akauliza.

“Yeah nimefanya uchunguzi wa kina na kila kitu kipo sawa, hata ulinzi huku si sana kama mjini,” Amanda akawaambia swahiba zake.

“Good!”Martin akajibu na kujitupa kitini.

“Sasa ni kuoga na kulala mengine kesho asubuhi, ratiba ipo vipi Amanda?” Martina akauliza.

“Aaaannh kesho kuanzia majira ya saa tano asubuhi hivi, viongozi wataanza kuingia hapa jijini tayari kwa mkutano wa kesho kutwa. Mpaka sasa katika orodha yangu, wageni wa ndani na nje tayari wametimia wote wanasubiriwa hawa wa juu tu ili kikao kifanyike,” akawaambia.

“Na kila kitu kipo sawa?”

“Kila kitu nimeweka sawa, tusubiri wakati tu, maana kazi yetu ni kesho kutwa baada ya mkutano,”

“Unaonaje, tutafanikiwa au la?”

“Tutafanikiwa tu, ila tu inabidi tuwe na chaguzi mbili za kutekeleza mauaji ama kwa risasi au kwa sumu…”

“Usijali, kwa kuwa hiyo ni kazi yangu nitashughulikia mwenyewe, tukutane kesho hapa kwa chai na mipango mingine, pia lazima tufike uwanja wa ndege ili kuungana na wapenda amani kuwapokea viongozi wetu,” Martin akasema na wengine wakabaki kuangua vicheko.





WATERLOO – SIERRA LEONE

Kamanda Amata na yule mwanamke waliangukia mtoni, ilimchukua kama sekunde kumi na tano hivi kuibuka juu ya maji na kuanza kuogelea kwa ufundi huku akimsaidia yule mwanake ambaye alionekana kutoyamudu maji hayo yaendayo kasi ya Mto Lofa. Kwa maelekezo machache aliweza kuijiokoa kisha wote wakatoka nje yam to huo.

“Asante sana, umeniokoa!” yule mwanamke akashukuru.

“Unaitwa nani?” akamuuliza.

“Relindis!” akajibu huku akitweta kama mbwa aliyekimbizwa.

“Ok, tuondoke hapa hapatufai,” Amata akamwambia na kuanza kumkokota na kupanda mlima kwenda juu walipoacha lile gari. Baada ya dakika kama thelathini hivi wakalifikia gari lao na kuingia ndani.

“Wapi tunaenda sasa?” Relindis akauliza kwa shauku.

“We unataka twende wapi?”

“Kwangu!”

“No! kazi inayonikabili ni kubwa na ngumu sana, sina budi kuondoka nje ya nchi hii,” Amata akamwambia huku akiwasha gari na kulirudisha barabarani kisha akaliondosha kwa kasi.

“Safari hii umefikia wapi?”

“Hata safari ile sikucheck-out, hivyo nipo Swizz Spirit,” Amata akamwambia wakati tayari akiwa barabara kuu kuelekea Freetown. Mwendo wake haukuwa wa kawaida kwa maana alikuwa akishindana na muda, wakati gari hilo liko katika kasi hiyo Relindis alikuwa kimya kabisa akimwangalia kijana huyo anavyobadili gia na kupanga na kupangua.

* * *

Mbele ya hoteli ya Swizz Spirit iliyojengwa katika viunga vya mji wa Freetown, Amata aliegesha gari mita kama mia tatu hivi, akamtazama Relindis ambaye bado alikuwa ametota kwa maji ya mtoni.

“So?” akauliza mwanamke yule.

“Nenda nyumbani kwako kaendelee na mapenzi yenu na yule gabacholi, nipigie baada ya saa tatu hivi…”

“Si kukupigia, ninaingia kazini muda huo…”

“Basi utanikuta! Si unajua kuendesha gari?” Amata akamwuuliza.

“Bila shaka!” mwanmke huyo akajibu na kufungua mlango, akazunguka upande wa derevana kuingia huku akimwacha Amata kasimama kando, akaondoka zake. Baada ya kuhakikisha gari lile limetoweka kabisa katika upeo wa macho yake, Kamanda akavuta hatua mpaka ndani ya hoteli ile na kuingia chumbani mwake pasi na kujulikana na mtu. Baada ya kuoga na kuwa katika hali nzuri, akaketi kitandani na kuchukua ile karatasi ambayo sasa ilikuwa imelowa, akaifungua taratibu ili isichanike na kuiweka mezani kisha akawasha taa ya kusomea na kuruhusu joto lake liifikie karatasi hiyo angalau inyauke kidogo.

‘Addis Ababa, yote yakamilike!’

Karatasi ile ilikuwa imeandikwa kwa mkono, na maneno hayo ndiyo yaliyosomeka japo kwa shida kutokana na mfifio wake, kisha kukafuatiwa na namba kadhaa za simu ambazo kwa Amata hazikumsumbua kujua kuwa ni za Ethiopia, namba hizo hazikuwa na majina, hilo halikumfanya kushindwa kujua kuwa ni za simu. Akakumbuka maneno ya yule dereva.

“… mmoja alikwishaondoka na wawili ndo sasa nimetoka kuwapeleka Uwanja wa Ndege…”

Akatikisa kichwa na kutazama tena saa yake, ikamwonesha kuwa ni saa mbili usiku, akapita hesabu zake kama waliondoka muda ule basi bila shaka wamekwishafika Addis.

Niko nyuma ya muda, shabash!!! Akawaza huku akianza kukusanya vitu vyake na kuvitia begini.

No time to waste! Akazidi kujikuta akiwaza, akili na mawazo yake yote yalikuwa ni kumtia mkononi Martin Gupter, Fredy na yule mwanamke wao ambao mpaka dakika hiyo walikuwa wakitikisa vichwa vya wanausalama wa Afrika. Baada ya kuhakikisha kila kitu kimekuwa sawa na kimehifadhiwa vyema begini, akachukua simu yake na kuiwasha, ikawaka, akaingiza namba anazozijua na kuzipiga.

“TSA 1!” akaita na upande wa pili simu ile ikapokelewa.

“Adui wetu amekwishafika Addis Ababa, narudia, adui wetu amekwishafika Addis Ababa!” Amata akaongea kwenye simu hiyo.

“Umesomeka, mpango ukoje upande wako?” sauti ya upande wa pili ikauliza.

“Naelekea Addis sasa!”

“Vyema! Na tukutane Addis!”

Simu ikakatika, Kamanda Amata akainua begi lake na kutoka nje, katika meza ya mapokezi akakamilisha taratibu zote za kuondoka.





ADDIS ABABA – ETHIOPIA

SIKU HII TOFAUTI NA SIKU nyingine zote, pambazuko lake lilikuwa na mikiki mikiki mingi, wapo ambao hata hawakujali nini kinatukia siku hiyo, wengine hawakupata hata lepe la usingizi kwa kile ambacho walijua kinaweza kutokea, na hawakupenda kitokee, hawa hawakuwa wengine zaidi ya wanausalama wa taifa hilo na nchi nyingine za Afrika.

Vikao vilivyofululiza kwenye taasisi mbali mbali vilikuwa vikizungumzia swala hili; kikao cha kamati kuu ya AU pamoja na usalama wa viongozi hao kufuatia mauaji yliyotokea Angola, Ivory Coast na kukoswakoswa kwa mwenyekiti wa umoja huo, rais wa Gambia alipokuwa katika moja ya vikao vidogo vya umoja huo jijini Dar es salaam. Katika moja ya agenda ambazo zingezungumziwa katika kikao hiki cha kamati kuu, ni pamoja na kulifikisha katika muafaka swala la kuimega Somalia na kuwa mataifa mawili kama ambavyo watu fulani walitaka, na kwa kushinikiza hilo waliamua kufanya mauaji ya viongozi wa umoja huo.

Katika kikao hiki, kulitegemewa ugeni mkubwa wa tajiri mkubwa Afrika Bwana Jaffer Bakhari, aliyekuwa akitajwa na kila chombo cha habari duniani kuwa ni chanzo cha machafuko huko Somalia na mauaji ya viongozi wa Afrika. Katika kikao hiki alitakiwa kufika kwani agenda mojawapo ilimhusu yeye na Somalia yake.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Katika moja ya majengo nyeti ya serikali Mtaa wa Eritrea, kikao cha baraza la usalama la AU kilikuwa kikimaliza mkutano wake alfajiri hiyo.

“Ulinzi utatakiwa uwe mkali sana kama tulivyoamua, na wapelelezi wetu wahakikishe wanaiweka Addis katikati. Hawa washenzi hawatakiwi kupenya sehemu yoyote ile kuingia ndani ya jiji hili kwa maana madhara yao tunayajua…” alizungumza mwenyekiti wa baraza hilo wakati akifunga kikao.

“Samahani mwenyekiti, kama sijasahau, mjumbe wa Tanzania alisema wao wataendelea na sakata la kumsaka huyu au hawa wauaji kwa sababu walifanya tukio hilo ndani ya ardhi yao, swali ni je, huoni kuwa kama watafika hapa watavuruga upelelezi wetu?”

“Yule bibi aikuumize kichwa, hana lolote si yeye wala idara yake, nashangaa sana kwa nini AU iliwaamini kiasi hicho, lakini sasa wameona, wameshindwa…”

“Mwenyekiti, mpaka sasa tunajua Tanzania na idara yake imefikia wapi katika uchunguzi huu? Si ajabu wakawa mbele kuliko sisi, mimi nafikiri tyumhusishe mpelelezi mmoja wan chi hiyo kutoka idara yao ya kijasusi ili aungane na hawa wetu, tukifanya hivi tutafaulu…”

“Hakuna kitu kama hicho mjumbe! Mpaka sasa ninavyokwambia, mpelelezi wao wanaomtegemea amekwishakufa lakini wamefanya siri, na amekufa katika sakata hili hili,” akajibu kwa kumkata kauli mjumbe huyo. Wajumbe wa kikao hicho wakatazamana na kubaki na alama za kushangaa na kujiuliza; moja kiongozi wao kajuaje kama mpelelezi wa Tanzania amekufa? Na kwa nini wao hawana ripoti kama hiyo? Kwa sababu wao walichokuwa wakijua tu ni kwamba, idara ya ujasusi ya Tanzania imeshindwa kufanya kazi kwa wakati na kuwasilisha taarifa kwa muda muafaka, basi. Kwa ukimya ule mwenyekiti wa baraza akagundua kuwa amekosea kwa kusema hivyo.

“Sawa sawa wajumbe, tutaliongea hili katika kikao chetu cha jioni na mtapta jibu kama Tanzania itahusika au la,” akajaribu kuliweka sawa jambo hilo.

Hawa nao wakamaliza kikao chao na kutawanyika kadiri ya majukumu yao.

Mpaka kufikia saa tatu asubuhi hakuna hata mwanausalama mmoja aliyegundua uwapo wa Martin Gupter na kundi lake katika jiji hilo. Ijapowa upekuzi wa kina kwa kila mgeni ulifanyika lakini haukuza matunda.

“Wameogopa kuja!” mmoja wa makachero akamwambia mwenzake.

“Wanajua wakija watajichimbia kaburi,” mwingine akaitikia. Tayari Addis Ababa ilikuwa na pilikapilika nyingi siku hiyo kwa kuwa ni saa chache tu zilizofuata mgeni wa kwanza angefika katika nchi hiyo, hivyo tayari vijana walipangwa, dori kwa kutumia magari na helikopta zilikuwa zikifanyika.

* * *

Kutoka Sierra Leone, Uwanja wa ndege wa kimataifa wa Lungi, Kamanda Amata alifanikiwa kuabiri ndege ya saa saba usiku ya sirika la AIATA. Wakati wa safari yote hiyo alikuwa akiwaza tu ni jinsi gani atamtia mkononi Martin na kundi lake. Alijuwa wazi kuwa kuna timu iliyoundwa kwa ajili ya upelelezi wa watu hao, lakini yeye aliamua kutokuwaacha, bali kuhakikisha anawatia mbaroni au anawapoteza kwa mkono wake.

Saa mbili kamili asubuhi, ndege hiyo akakanyaga ardhi ya Addis’ kwa madaha na kuingia katika egesho lake, kisha wageni wakaruhusiwa kuingia katika jiji hilo. Miongoni mwa wageni waliofika asubuhi hiyo alikuwamo Kamanda Amata, akiwa ndani ya jinzi mpauko, shati la drafti nyekundu na nyeusi na kichwani mwake kofia kubwa ya pama, miwani ya kumkinga dhidi ya miale mikali ya jua ilitulia vyema machoni pake aghalabu ndevu bandia zilimfanya afanane na cowboy mmoja hivi. Kifuani mwake alining’iniza kamera ya kisasa kabisa, kama ungemtazama usingefikiria zaidi bali ungejua tu kuwa ni mwandishi wa gazeti fulani la kimataifa. Kwa uzoefu wa kazi yake aliweza kuwana makachero wengi uwanjani hapo, lakini wao hawakuweza kumgundua kirahisi labda kwa sababu hawakuwa na mpango naye. Nusu saa baade alikuwa katika hoteli kubwa ya Blue Moon, katikati ya jiji hilo. Hakutaka makuu zaidi ya kutulia kimya chumbani kwake na kupanga hili na lile kwa maana alikuwa akijua wazi kuwa viongozi wanaotegemewa wataingia nchini hapo siku hiyo na mkutano huo utachukua nafasi siku inayofuata.

* * *

‘Hakikisheni mnawatia mbaroni, wao watatu na wengine wapo hapahapa tunaendelea kuwalinda, mambo yakiwa tiki tu tunawapiga pingu. Msiwe na wasiwasi na mimi, mimi naendelea poa kabisa na naweza nikatoka hospitali muda wowote kutoka sasa. Chiba na Gina mfike Addis haraka iwezekanavyo, nafikiri kaka yenu keshafika huko, nendeni mkafanye yale mnayopaswa kutenda.’

Chiba wa Chiba alikuwa akikumbuka maneno ya bosi wake, Madam S, mara walipokuwa wakiagana katika hospitali ya jeshi ya Lugalo. Mwanamama huyu hatari kabisa katika medani za kiusalama alilazwa hospitalini hapo siku tatu nyuma baada ya kupata ajali mbaya ya gari katika makutano ya Barabara ya Morogoro na Bibi Titi. Mara baada ya kupata taarifa kutoka kwa Amata kuwa ‘wanawatafuta’ wapo Ethiopia, akaamua kuongeza kikosi katika jiji hilo, hivyo TSA 2 na TSA 5 waliingia kazini.

“Tumefika!” Chiba akamwambia Gina. Gina akatupa jicho dirishani na macho yake yakapendezeshwa na mandhari ya kuvutia ya Jiji la Addis Ababa.

“Ni mara yangu ya kwanza kufika hapa,” Gina akamwambia Chiba.

“Safi sana nitakupeleka ukale injera,” akamtania. Injera ni chakula cha kienyeji katika nchi hiyo kama ilivyo kwetu ugali. Mara sauti ya kike ikawataka kufunga mikanda nao wakafanya hivyo tayari kwa kutua. Akaitazama saa yake, ikamwambia kuwa tayari imetimu saa sita mchana. Wakiwa katika harakati hizo wakapata tangazo lingine la dharura ya kuwa watasalia angani kama dakika arobaini na tano hivi ili kupisha ndege za marais wa Gambia na Afrika Kusini kutua.

“Kumekucha!” Gina akasema.

“Kwa vipi?”

“Sipati picha rafiki zetu jinsi wanavyohaha sasa kwa mapokezi hayo,” akasema akimaanisha wanausalama wa nchi hiyo. Baada ya saa moja hivi ndege ile ikatua katika uwanja huo mkubwa kabisa wa Bole.

“Kazi ya kwanza!” Gina akamuuliza Chiba mara baada ya kutoka nje ya uwanja huo.

“Kuweka mipango yetu sawa, tunatakiwa kufika katika shamba la kanisa la Orthodox, mambo yetu yote yatakuwa huko,” Chiba akamwambia Gina, na wakiwa katika mazungumzo hayo, gari moja, Toyota Pickup likasimama umbali wa kurusha jiwe tu utoka wao waliposimama. Ndani ya gari hilo kulikuwa na mwanaume mmoja aliyevali kanzu jeusi na msalaba mkubwa kifuani mwake, akafungua mlango na kutoka nje. Alipowaona tu Gina na Chiba, akainama kama ishara ya kuwasalimu nao wakafanya hivyo hivyo, moja kwa moja wakajua kuwa huyo ni mwenyeji wao wakaongozana na kuingia garini.

“Karibuni Addis!” yule bwana akawakaribisha huku tayari akikamata barabara ya kuelekea nje ya mji, “Naitwa Archemedius, kutoka Orthodox Church,” akajitambulisha.

“Asante sana,” nao wakajibu na kujitambulisha kisha mazungumzo mengine yakafuatia ambayo zaidi yalikuwa na kufahamiana na kujuliana hali. Baada ya mwendo wa takribani saa moja na nusu hivi, waijikuta nje ya mji. Yule bwana akaiacha barabara kubwa na kuchukua ile ya vumbi yenye mashimo na machanganyiko wa mawe na udongo. Kilomita moja mbele wakaingia kwenye wigo wenye kanisa kubwa sana mbele yao, gari likatembea taratibu mpaka ndani ya kijumba kimojawapo. Wakateremka na kuchukua mikoba yao kisha wakamfuata yule mwenyeji wao. Wakapita kando ya kanisa hilo na kukutana na ukuta upande wa nyuma, wakauzunguka mpaka upande wa pili ambapo palikuwa na mlango mdogo wa chuma. Yule kasisi akabofya sehemu fulani ya ukuta na sekunde kumi tu zilizofuata kijimlango kile kikafunguka, wakaingia ndani.

Ulikuwa ni uwa mkubwa sana, wenye maua mengi ya kupendeza, kwa harakaharaka utavutiwa na ukimya wake, hapakuonekana mtu, bali vipepeo tu vilivyokuwa vinaruka huku na huko. Archimedius, akawafikisha kwenye moja ya milango mingi na kuufungua, wakaingia na kujikuta kwenye kijichumba kidogo. Chiba akatazama harakaharaka na kugundua kuwa ilikuwa ni lifti, ikawateremsha chini kama mita kumi na mbili hivi, wakatoka na kupita koridoni mpaka katika chumba kingine.

“Karibuni sana!” Archimedius akawakaribisha kwa mara ya pili wakiwa wanajibwaga kwenye makochi ya kisasa kabisa yenye vono ya kuvutia, “Jisikieni mpo nyumbani, Madam S ndiye aliyeuagiza tuwafikishe hapa na kuwapa sehemu ya kuratibu kazi zenu, hivyo mpo sehemu salama sana. Hii sehemu watu hawaijui na wala hawajawahi kufika, kama mnavyoona ni kanisa ambalo hutumika kila jumapili na huko juu kuna monastery kubwa ya kimisionari ya Orthodox ya Mtakatifu Ilarius,” akawaeleza.

“Hapa tulipokaa kuna vyumba vitatu, hili siyo jokofu ni mlango wa chumba, ukibonyeza namba 0-7-7-3, utaingia chumbani,” akachukua rimoti mezani na kubofya namba hizo, kweli, ule mlango ukafunguka na ndani yake kulikuwa na kitanda kikubwa, meza ya kujiremba, na kabati moja la nguo, kiti kimoja na meza ya kusomea.

“Lakini ukikose na kubonya namba nyingine yoyote ile, utafungua jokofu na si chumba,” akafunga ule mlango na kubofya tarakimu nyingine hapo ukafunguka mlango ule ule lakini mara hii vilionekana vinywaji na matunda na vyakula anuai.

“Du! Hii nimeikubali!” Gina akajikuta anamwambia Chiba, naye akatikisa kichwa kuonesha hiyo ni ‘kali ya mwaka’. Yule kijana akawatazama Gina na Chiba na kuendelea kuwapa maelekezo, “Na chumba kingine ni upande huu, hilo hapo si kabati la vyombo, ni chumba na namba yake ni 7-3-2-0, kama mwanzo, ukikosea utakutana na mabakuli na vijiko. Na cha tatu ni hiki huku kwenye shelfu la vitabu namba yake ni 6-7-0-5. Kwa hiyo mkariri hizo namba, mambo yenu yote mtayafanyia hapa ndani, hakuna atakayewasumbua hata mimi tukiachana hapa hamtaniona tena, baada ya hapa njooni niwaoneshe jambo la mwisho,” akawachukua na kutoka nao kwenye ile korido, wakaifuata na kuingia kwenye lango kubwa, huko kulikuwa na eneo wazi kubwa lililoegeshwa magari mengi sana katika mpangilio wa kupendeza.

“Hapa ni maegesho, mkitaka kwenda mjini, mtachukua gari hapa mnayoipenda, funguo zipo ndani na ukifuata hiyo mishale itakutoa nje ya mpaka mjini, nimemaliza!” Archimedeus akamaliza kuwapa maelekezo na kurudi nao ndani.

“Samahani nilisahau jambo, mkimpata mwenzenu, mtamleta hapa, kazi yenu haitakiwi kupangwa nje ya chumba hiki, kwa maelekezo niliyopewa,” akamaliza na kupeana nao mikono kisha wakaachana. Gina na Chiba wakarudi ndani ya kile chumba na kuufunga mlango, kila mmoja akajaribu rimoti kufungua chumba chake na kuingia. Kila chumba kilikamilika, choo, bafu ndani na jiko dogo la kahawa au chai lilikuwepo.

Chiba akarudi sebuleni na kuwasha luninga kubwa iliyowekwa ukutani, macho yake yakakutana na matangazo ya moja kwa moja kutoka kituo cha televisheni cha EBC. Hakikuwa kingine ni mapokezi ya marais waliokuwa wakimiminika katika jiji hilo.

* * *

Hoteli ya BLUE MOON

Kamanda Amata bado alikuwa ametulia kimya katika chumba chake hicho, huku mezani kukiwa na chupa kubwa ya pombe aina ya Covousier ikiishia tumboni mwake taratibu, makwapani mwake alikuwa amening’iniza bastola mbili, mja upande huu na nyingine upande mwingine. Kwa ujumla alikuwa tayari kwa kazi lakini bado akili yake haikuwa katika umoja mzuri na mwili wake. Katika meza hiyo hiyo, alikuwa ameweka kijitabu kidogo cha kumbukumbu, si chake bali kile alichokichukua kwa marehemu Innocent na karatasi nyingine ile aliyoichukua kule Waterloo ndani ya jumba ‘Silent Rock Villa’. Ukiachana na mkono ulioshika bilauri iliyojaa pombe nusu, alikuwa amekamata simu upande mwingine akibofya namba ambazo amezikuta zimeandikwa ndani ya karatasi ile. Katika hisia zake, kwa vyovyote, alijuwa wazi kuwa wenye namba hizo watakuwa na uhusiano na Gupter na kundi lake ama wa kikazi au wa kidugu.

Nitajitambulishaje? Akajiuliza mara baada ya kuiweka simu sikioni na kusikia ikiita upande wa pili. Simu yake hii ilikuwa ni ile ambayo ni vigumu sana kuitambua uelekeo ilipo.

“Hello!” upande wa pili ikaitikia.

“Bole International Airport, reception, habari za kazi!” Amata akajikuta akitamka kuwa simu hiyo inatoka katika meza ya mapokezi ya Uwanja wa ndege wa Bole.

“Kuna mtu hapa ni mgeni wako ametupatia namba hii ili uje umpokee, amefika takribani saa tatu zilizopita, tafadhali fika mapokezi umchukue!” Amata akasema huku ahajui nini atafanya kama aliyempigia simu atakubali wito huo.

“Ok, got’ya!” upande wa pili ukajibu na simu ikakatika.

“Bingo!” Amata akajikuta anasema kwa sauti, akainuka na kujitupia koti lake ili kuficha ile ‘miguu ya kuku’, akainuka na kuitia ile simu mfukoni, akachukua vitu kadhaa ikiwemo kile kijitabu cha kumbukumbu ambacho hakukiacha hata nukta moja tangu akipate kwa maana hakuwa amemaliza kazi yake. Akafungua mlango na kutoka nje, akashuka chini kabisa ya hotei hiyo na kuzielekea taksi, moja wapo ya hizo ikamchukua na kumkimbiza uwanja wa ndege.

* * *

Katika kitongoji cha Aleltu, nje ya jiji la Addis kilomita takribani hamsini na tatu kutoka mjini kati, ndiko Martin Gupter na kundi lake waliweka makazi ya muda ambayo kwa mipango yao, hayo yalikuwa makazi ya saa tisini na sita tu. Mwendo wa nusu saa tu ungeweza kufika katikati ya jiji hilo kama ungeendesha gari kwa mwendo kasi wa kilomita 100 kwa saa.

Martin Gupter aliteremsha kikombe chake cha kahawa huku macho yake yakiwa kwenye dirisha kubwa yakisanifu mandhari ya nje ya nyumba hiyo. Nyumba hiy, Amanda alikuwa ameikodi kwa juma moja tu kwa ajili ya kufanyia kazi yao, alikwishaihakikishia usalama, kwa kuwa ni mara nyingi wageni wan je huitumia kwa kuikodi kama wao. Ikiwa ni moja ya mbinu za kujificha kwa kivuli cha watalii ndani ya jiji hilo maarufu kabisa Afrika. Kwa mbali katika barabara ya vumbi aliliona gari likija kasi upande huo, akachukua darubini yake na kutazama. Ni gari ambalo haikumchukua muda kulijua.

“Amanda amefika!” akamwambia Fredy, kisha wakatoka nje kumlaki, dakika moja baadae wote wakawa tayari wameketi kuizunguka meza moja ya duara sebuleni hapo.

“Tupe habari za mjini!” Martin akaanzisha mazungumzo.

“Huko ni moto asee, kama nilivyowaambia jana, wageni wetu wameshaanza kufika, na wote tayari ninajua wapi wanafikia, isitoshe hata wana uinzi kiasi gani…”

“Wanapenyeka?” Fredy akadakiza swali.

“Itabidi wapenyeke, hakuna jinsi,” Amanda akasisitiza huku akijimiminia kahawa, na alipomaliza na kupiga funda moja akakitua kile kikombe.

“Mmepata taarifa yoyote kutoka kwa mteja wetu?” Amanda akatupa swali maana anajua kuwa taarifa nyeti za kazi huwa zinafika moja kwa moja kwa Martin na si mtu mwingine yeyote.

“Yes! Ujumbe wote utafika jioni ya leo, utakuwa na watu sita akiwamo Fadick Al Habib, na ndiye kiongozi wa msafara, mzee mwenyewe hawezi kufika wala wenzake. Maagizo ni yale yale, mkutano wa AU na hawa jamaa utakuwa saa tisa alasiri jioni, wakikubaliana basi kazi imekwisha, wasipokubaliana tunatakiwa tuendelee na operesheni yetu. Sasa endapo itatubidi tuendelee na operesheni, ndiyo tupange sasa…!” Martin akawaeleza.

“Sawa, baada ya kikao cha kesho, usiku kutakuwa na tafrija katika hoteli ya kifahari ya Golden Tulip, na hawa wageni wote watakuwepo,” Amanda akatoa maelekezo.

“Nimekuelewa, sasa baada ya kazi ya kesho sote tunatakiwa tukutane na Jaffer kule Riyadh kwa bakshisi za mwisho…” Martin akawaambia na kila mmoja akatabasamu.

“Sasa nafikiri ni muda muafaka kutoka, cha muhimu ni kujiweka sawa, tusitambulike, tukaikague hoteli hiyo, na ile atakayofikia mwenyekiti wao kisha tutazame na mengine ii siku ya kesho tuwe tayari,” Martin akamaliza kwa kuwaambia hilo na kila mmoja akaanza kujiandaa kwa jinsi anavyojua yeye ili mradi tu wakiwa huko mjini basi wasigundulike kirahisi.

* * *

Uwanja wa ndege wa BOLE

Kamanda Amata akawasili katika uwanja huo, akaiacha ile taksi baada ya kumaliza kulipia huduma hiyo, akavuta hatua na kuyapita maegesho mpaka kwenye sakafu ya uwanja huo. Macho yake yalikuwa yakipepesa harakaharaka na kutazama huku na huko, ni hapo ndipo ailipokutana macho kwa macho na mtu asiyemtaraji; kijana jamali, mweusi wa wastani mwenye tambo haswa la kipiganaji ambalo lilifichwa na nguo nadhifu, suti ya kisasa ambayo isingeweza kumpa wasiwasi mtu yeyote amtazamaye.

Drunken Hamidou, mpelelezi kutoka jumuia ya ECOWAS, akamsalimu kwa macho pasi na kumkaribia kwa maana alijua kwa nini mtu huyo yuko hapo. Almwona wazi kuwa kijana huyo alitamani kumkaribia na kumsalimia, kwa jinsi alivyopigwa na mshangao lakini Amata hakuruhusu hilo kwani yeye alikuwa na kazi yake binafsi. Akamwacha na kukaribia meza ya mapokezi ambako kwa ndani kulikuwa na watu wawili na nje kulikuwa na mtu mwingine ambaye kulionekana kama kuna mabishano kati yao. Akili ya Amata ikafanya kazi haraka na kujua kwa vyovyote alichokitaraji ndicho kinatokea. Naye akawasili palepale mezani na kujifanya akiongea na mhudumu mwingine kuuliza maswali ambayo hayana jibu la kiurahisi. Huku akisikiliza mazungumzo ya watu wale wawili wakibishana, huyu wan je akisema kuwa amepigiwa simu na amekuja kumfata mgeni wake, na huyu wandani akipinga kuwa hawajapiga kwa mtu yeyote kuhusu huo ugeni. Mwishowe yule kijana mwenye asili ya Uzungu uliyochakaa akaondoka akitukana matusi. Kamanda Amata akamalizana haraka na mhudumu huyo na kuondoka, lengo lake halikuwa jingine zaidi ya kumfuatilia mtu huyo. Akamtazama akielekea katika maegesho, huku akiongea kwa simu yake na kusimama nje ya Range Rover moja ya gharama sana. Kamanda Amata akajifanya kama anafunga kamba ya kiatu chake ili kumpa nafasi kijana huyo kumaliza mazungumzo yake.

Kijana yule hakuwa na hili wala lile, aliposhusha simu yake, na kuitia mfukoni, akageuka kukamata mlango wa gari ndipo akajikuta ana kwa ana na domo la bastola, mtu aliyekamata mashine hiyo hakuwahi kumwona hata siku moja tangu azaliwe.

“Uphhhhhhh!!!!!” akashusha pumzi na kijasho chembamba kikaanza kumtiririka.

“Ingia!” Amata akamwambia kwa kiingereza.

“Wewe ni nani…?”

“…Get in!!” akamwambia tena huku tayari akiwa keshaondoa kilinda usalama cha bastola hiyo. Yule kijana akafungua mlango na kuingia na Amata akaingia mlango wa nyuma yake na kuketi, mara hii akamwekea mtutu wa bastola kwenye mbavu zake upande wa nyuma.

“Drive!” akamwamuru.

“Tunaenda wapi?” yule kijana akauliza.

“Nyumbani kwako!” akamjibu.

“Nyumbani kwangu?” akauliza, “Mi sina nyumba, kama unataka gari chukua!!!” yule kijana akaongea kwa kitetemeshi huku akimpa funguo Amata.

“HEYYYY!!!!” Amata akang’aka, na yule bwana akabaki kimya kabisa.

“Bosi wako ni nani?” akamtupia swali.

“Mr. Bbaattolloommiinno!!” akajibu huku akitetemeka.

“Nina shida na yeye, nipeleke!” akamwamuru.

“Ssaawwaa!!” akajibu na kuwasha gari, Amata akatulia kimya akimwangalia kijana huyo akiendesha kwenye barabara za Addis kuelekea huko atakako. Kijana yule ambaye kwa kumwangalia na kumsikia lafudhi yake tu ungejua kuwa ni Mtaliano aliendesha gari kwa takribani dakika kumi hivi na kuufikia Mtaa wa Lorenzo Tiezaz, hapo akaachana na barabara ya kwanza na kuingia kwenye mtaa huo mpaka katika jumba moja kubwa lenye wigo mkubwa sana wa michongoma.

“Ni hapa!” yule kijana akamwambia Amata.

“Sikiliza, mimi ndiye mgeni wake ambaye ulitakiwa kunifikisha kwake, na nimefika uwanja wa ndege kwa saa nyingi sana, sasa nipeleke nionane naye,” akamwambia na dakika hiyo hiyo lango likafunguka na lile gari likapotelea ndani ya kasri hilo. Mbele ya jumba hilo, alisimama mwanadada mrembo wa kizungu, akisubiri gari hilo kuegeshwa.

“Umefika, na huyo mwanadada atakufikisha kwa Bwana Mkubwa!” yule kijana akamwambia Amata.

“Asante, unisubiri hapa ili unirudishe, sawa?”

“Sawa!”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Amata akashuka na kupeana mikono na yule mwanadada, kisha akaongozwa ndani ya jumba hilo mpaka kwenye chumba kimoja cha gharama sana, akaingia na kukaribishwa na mzee wa makamo, mnene, aiyejaa kwenye kiti alichokikalia.

“Karibu sana!” akakaribishwa huku yule mwanadada akimimina kinywaji kikali bilaurini.

“Asante sana! Nimeshakaribia,” Amata akajibu na kujituliza kitini.

“Nimepata simu kuwa wewe ni mgeni wangu,na mimi sikutegemea ugeni siku ya leo,” yule bwana akamwambia Amata.

“Ndiyo, na mimi ndiye niliyepiga simu, si kweli kwamba ilipigwa kutoka uwanja wandege,” akamwambia.

Maneno hayo yakamfanya yule bwana ashtuke kidogo, maana hakuelewa imekuwaje hata mgeni huyu apige simu na kufika mahala hapo. Akamtazama mzungu yule, Mtaliano mwenye nywele nyeupe zilizomwagika mabegani kama za Sir Newton Isaac.

Hawa ndiyo mabaki ya Wataliano walioua ndugu zetu Waethiopia miaka ileee! Amata akawaza, akijaribu kuirudia historia ya watu hao walipoingia katika nchi hiyo na kufanya mauaji mabaya kabisa ya ‘weusi’ zaidi ya elfu ishirini au thelathini.

“Enhe, nipe ujumbe wangu kijana maana huwa sina muda mrefu wa kuzungumza na watu hasa wasio na miadi kama wewe!” akaongea kwa dharau huku akiweka mtemba wake kinywani na kupiga pafu kama tatu hivi na kuruhusu moshi mzito ukijaze chumba hicho kupitia tundu za pua yake kubwa.

“Tunaweza kubaki wawili?” Amata akamuuliza.

“Bila shaka!” akajibu na kumwamuru mwanadada yule atoke, naye akafanya hivyo.

Kamanda Amata hakuzungumza, akachomo picha tatu mfukoni mwake na kumwekea mezani. Yule mzee akazitazama kwa makini, kana kwamba kajua ni nini ambacho mgeni wake huyo atasema. Akachukua tena mtemba wake na kuuweka kinywani, akapiga pafu kadhaa na kuushusha kisha akakung’uta jivu kwenye kibweta chake. Kwa mkono mwingine akaichukua picha ya mwanamke, Amanda, akaiweka kando.

“Namjua huyu!” akamwambia Amata. Moyo wa Amata ukapiga samasoti, akahema kwa nguvu, “Vipi una shida naye?” yule bwana akauliza na kumgutua Amata kwenye lindi la mawazo.

“Unamjuaje? Ninamhitaji kwa hali na mali,”

“Huyu ni mteja wangu, nimemwona si mara nyingi, bali alikuja hapa kukodi nyumba ya kuishi kwa muda wa wiki moja hivi…”

“Una nyumba za kukodi?”

“Si! Si! Nyingi sana, nimezijenga mashambanai huko,” akaeleza.

“Nahitaji kukutana naye, nipe maelekezo,” Amata akamwambia.

“No! siwezi kukupa maelezo yoyote ya mteja wangu, ni kinyume na baishara hii,” Balomino akajibu.

“Utanipa au hutonipa?” Amata akamuuliza.

“Nikupe wewe kama nani?” yule Mtaliano akauliza huku akijiweka vyema kitini, Amata akaigundua hila yake, kwa wepesi sana akainuka pale alipo na kumbana yule mzee kitini, kisha akachomo bastola kutoka kiunoni mwake, akarudi na kujibwaga katika kiti chake huku akiwa kamnyoshea mtaliano huyo domo la Berreta 87, bastola ya kizamani ya miaka ya ’76 huko Italia na wengine huuita ‘Series 81’.

“Niambiye hiyo nyumba ipo wapi?” akamuuliza, yule bwana kijasho kilikuwa kikimwagika.

“Aleltu!” akajibu na mara mguu wake ukakanyaga kitufe fulani chini ya meza. Amata akajua mambo yashaharibika, sekunde yoyote wangemvamia hapo, akatazama huku na huku.

“Hah! Hah! Hah! Hah! Aaaaaa!” yule tajiri akacheka cheko baya sana lililomuuzi Amata, akageuka na pigo moja zito akamzimisha kisha akafungua mlango, alipotaka tu kutoka akakutana na watu kama wane hivi wanakuja wakikimbia na bunduki mikononi. Akageuka na kurudi kwenye dirisha kubwa, huku mlangoni akiwa kasukumia kochi kubwa, akatazama huku na huko na kulifungua dirisha lile, akatoka na kutua nje.

Kumwacha hai si jambo zuri ataniharibia kazi! Akawaza na kuchukua ile bastola mkononi, akafyatua risasi moja iliyotua moyoni na kummaliza. Akaambaa ambaa na ukuta mpaka dirisha la tatu hivi, akalikuta lipo wazi, akachungulia ndani akamkuta mwanamke mmoja akiendelea na kazi kwenye kompyuta, akalikamata na kuingia ndani akatua bila kusikika. Akauendea mlango, na hapo ndipo yule mwanamke alipogundua kuwa hayupo peke yake, akapiga kelele lakini Amata akamuwahi na kumbana kinywa.

“Nipe ramani ya kufika Aleltu, kwenye nyumba za bosi wako,” akamwambia na kumwachia. Yule mwanamke akapekua na kumpa kitabu kimoja kikubwa tu lakini kinachoweza kuingia katika mfuko wa ndani wa koti lake.

“Nisindikize mpaka nje ya jingo,” akamwambia, na yule mwanamke akafanya hivyo, wakapita pamoja kwenye korido kana kwamba ni moja ya wateja wa tajiri huyo. Alipofika nje, akaagana na mwanamke huyo na kuingia kwenye gari lile lile lakini mara hii halikuwa na dereva ila funguo ilikuwa ikining’inia. Kamanda Amata, akaingia ndani na kutia injini moto, mashine ikaunguruma, akatingiza gia ya kwanza na kuondoka kwa fujo. Katika lango la kutokea nje mlinzi alizuia gari hilo lisitoke lakini mwenyewe hakuwa na budi kutoka barabarani baada ya kuona hakuna dalili za kusimama. Amata akagonga geti na gari lile likaharibika vibaya huku likiacha lango wazi. Akaendelea kuendesha kwa mwendo wa kasi mpaka sehemu alipoona panafaa, akasimama na kuteremka, akaliacha gari hilo na kuingia kwenye kichaka cha miti, akapotelea zake kwa mwendo wa miguu.

* * *

Chiba alikuwa mezani kimya huku kompyuta yake ikiendelea na kazi ya kutafuta mambo mbalimbali ikiwemo kuingia katika mitandao mbalimbali, lakini licha ya yote hayo alikuwa akijaribu kumtafuta Kamanda Amata kama anaweza kupata ishara yoyote. Wakati huo Gina hakuwepo humo ndani, yeye alijitoma mitaani kutafuta hili na lile ili baadaye wakijumuisha tafutishi zao waweze kupata kipi ni kipi. Chiba na Gina hawakuwa na muda mrefu wa kujua nini cha kufanya, kazi kubwa kwao ilikuwa ni kutegua kitendawili cha kama Martin Gupter na kundi lake wapo ndani ya Addis au la. Mpaka dakika hiyo kila ambako mashushushu wan chi hiyo walikuwa wametega kuwanasa, hawakuwaona.

“Sidhani kama wamefika” – labda ni maneno ambayo wanausalama wengi ambao wamejawa uvivu wa kiupelelezi. Sifa ya kuwa mpelelezi hasa kwenye kiwango cha espionage, lazima uwe na milango sita ya fahamu yaani umzidi mwanadamu wa kawaida. Wakati wao wanafuata wanayoambiwa na wakubwa wao tayari TSA walikuwa Addis na Kamanda Amata yupo hatua mbili mbele kuwatia mkononi washenzi hao.

Simu ya Gina ikaita, akainyakua kutoka kwenye mkoba wake, akaitazama kwenye kioo, kisha akasonga kando pasipo na watu na kuiweka sikioni.

“Uelekeo wapi?” sauti ya Chiba ikasikika kutoka upande wa pili.

“Katikati ya Mtaa wa Mauritius!”

“Kuna lolote?” akauliza.

“Upande huu hamna jipya, nimejaribu pia kupita HQ ya AU nako bado inaonekana hakuna jibu jipya, baadhi ya watu wanaofananishwa na Gupter wamewekwa tunduni, kiujumla hali ni tete,” Gina akaeleza.

“Vipi upande wako?” akamtupia swali.

“Huku habari ni nzuri, nimepata uelekeo wa Kamanda Ama….”

“Yeeeessss nambie yuko wapi?” Gina akamkatisha Chiba kwa furaha.

“Namuona karibu na Mtaa wa D.A.R Sahara, akielekea katikati ya mji,” Chiba akamuelekeza Gina, naye akawasha kifaa chake mfano wa simu ya mkononi na kuiweka juu ya kioo ramani ya Addis Ababa, akautafuta mtaa mtaa huo na kuupata kisha akatafuta barabara ya kufika kutoka pale alipo, akapata umbali ni k.m 9. Akaingia garini na kuwasha, kisha akingiza gari barabarani na kuufuata Mtaa wa Mauritius, akauacha ule wa Tanzania na kukunja kuchukua Barabara ya Ethio China.

Kwenye kompyuta ya Chiba aliweza kuwaona wote wawili na alijaribu kumuelekeza Gina jinsi ya kumkuta Amata, lakini baadae akashangaa kuona Gina amesimama mahali kwa muda mrefu sana. Akampigia simu na kujibiwa kuwa alikuwa amekamatwa na askari wa Barabarani kwa kuwa aliingia barabara kuu kimakosa. Chiba alijikuta akishikwa na hasira kwa kuwa muda ulikuwa ukipotea. Baada kama ya dakika thelathini hivi simu yake ikaita, akaipokea na kuzungumza machache na Gina.

“Sasa nenda hoteli ya Blue Moon ameingia hapo! Nafikiri ndipo alipofikia, ukimpata hakikisha unamhamishia huku,” Chibna akampa maelekezo Gina.

“Copy!” Gina akajibu na kukata simu.





ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog