Search This Blog

Friday 18 November 2022

KUFA NA KUPONA - 4

 






Simulizi : Kufa Na Kupona 
Sehemu Ya Nne (4)




"Kwa nini hukukataa?"



"Kwa sababu angeweza kuniua hata mimi, ndiyo alinitisha."



"Ulimuona mtu aliyemuua yule mtu aliyekufa pale ukumbini."



"Hapana sikumuona, lakini nilifikiria wewe unajua."



"Kwa nini ulichukua bastola nilipogonga mlangoni."



"Kwa sababu nilikuwa na wasiwasi juu ya mambo niliyokuwa nimeambiwa na Benny."



"Huwa unakaa na bastola hapa kwako, ama umepewa leo tu kuitumia.?"



"Nilipewa na Benny niitumie iwapo nitafuatwa na mtu yeyote."



"Kuna mtu mwingine yeyote anayeshirikiana na Benny?"



"Sijui hajaniambia lakini nafikilia huenda yupo, maana baada ya Lulu kuingia kwenye jukwaa leo, Benny alienda kupiga simu."



"Kuna watu wangapi waliotumia hiyo simu leo tulipokuwa kwenye maonyesho?"



"Ni Benny tu niliyemuona"



"Nambari ya simu aliyotumia Benny ni ngapi?"



"Una maana alikokuwa akipiga ama ile aliyokuwa anatumia?"



"Nina maana zote."



"Alikokuwa akipiga sijui, lakini ya mle mwenye 'hall' ni 21899."



Niliwambia wafunge midomo yao, mpaka baada ya siku mbili hivi. Nilionelea niwaache hivyo ningemwambia Robin aje awachukue awaweke ndani kwa siku mbili hivi."



"Haya wajomba, kama mnataka usalama fanyeni kama nilivyowaambia, na ujanja wowote, mnaweza kujikuta mko ndani zaidi. Na ndipo mtalia na kusaga meno." Niliondoka nikawapigia Sammy na Robin simu. Nilimweleza Robin juu ya hawa watu na jinsi ya kuwafanya. Akasema angefanya kama nilivyomwambia. Na pia akanieleza anahisi kupata fununu ya jambo fulani kwa hiyo lazima nimwone asubuhi hotelini kwake mnamo saa tatu hivi. Pia nilimweleza kuwa sasa naenda kumwona Lulu na nikamwambia Sammy apige huko hotelini kwa Lulu simu itimiapo saa nne hivi. Na kwamba ikifika saa nne na nusu bila ya kuniona aje huko hotelini kwa Lulu, huenda nitakuwa nimo msambweni.



Nilipiga simu kwenye Idara ya Uchunguzi nikawaeleza wanitafutie nambari za simu ambako simu ilipigwa kutoka kwenye simu nambari 21899 mnamo saa kumi na mbili na nusu. Na wakasema hiyo ni kazi rahisi. Pia niliwaambia wanipe jina la mtu mwenye simu hiyo, wakasema pia kuwa hilo lisinitie shida ni kazi ndogo.



Basi hatimaye niliondoka kwenda Hoteli Intercontinental. Nilipokuwa naingia nilimkuta Peter na Wazungu fulani fulani pamoja na wapigania uhuru wengine wakinywa kahawa katika chumba cha kahawa. Aliponipungia mkono nikaenda kuwasalimu. Nilikuta Wazungu wote hao walikuwa Marekani na walikuwa wanatoka katika Baraza la Umoja wa Mataifa, kwenye sehemu inayoshughulika na Afrika Kusini. Ilionekana walikuwa wamekuja kwa mazungumzo na wapigania uhuru.



Walininunulia kahawa, baadaye Peter na hao wageni wake iliwabidi waondoke wakalale maana walikuwa wamechoka. Nilimwuliza Peter kama amemwona Lulu, akasema alimwona akiingia ndani, lakini hajatoka nje. Pia nilimwuliza kama kuna mtu mwingine yeyote aliyekuwa ameingia na Lulu, akasema hakumwona yeyote. Basi tuliagana wao wakaenda zao miye Willy, nikakaza roho kupanda chumbani kwa Lulu.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Vijana wa Robin walikuwa wameishapata hata nambari za chumba cha Lulu. Nilienda moja kwa moja mpaka kwenye kile chumba. Lakini kwanza nilihakikisha hakuna mtu aliyeniona huko juu.



Hoteli Intercontinental ni nzuri sana na ghali. Na kama wee ni 'giriki' nusunusu huwezi, na msichana Lulu anatisha maana mtu wa kukaa katika hoteli hiyo lazima awe 'giriki'hasa. Hiyo ninaweza kusema kwamba Lulu ni 'giriki' hasa, ila sivyo asingeweza. Maana wanawake wengine wote wa kwenye maonyesho hata waliotoka ng'ambo ni yeye tu anayekaa hapa. Na kama kuna mtu aliyempangishia, lazima huyo mtu awe na pesa si mchezo. Na hii nadhani ndiyo ilikuwa kweli hasa, maana Lulu alikuwa msichana mrembo hasa. Mtu yeyote mwenye fedha angemfanyia lolote analotaka. Ninaamini kwamba, Lulu akikuambia wende ukamwibie fedha ili awe wako, Wallah utakubali ufungwe ikiwa utashikwa, lakini ukaibe.



Nilipofika kwenye kile chumba niligonga mlango. Ulifunguliwa na Lulu huku akitabasamu "Karibu ndani, mbona unakuja kunitazama usiku hivi? Nadhani mchana lingelikuwa jambo zuri zaidi." Alikuwa akisema maneno yote haya huku amenishikilia mkono mpaka kwenye sofa.



"Uh, naweza kukusaidia?"



"Maonyesho yako yamenipendeza sana mpaka imenibidi nije nikupe heko usiku huu," nilijibu. "Asante sana Joe nimefurahi kuwa umeweza kupendezwa na maonyesho yangu ukiwa kama mwandishi wa habari."



"Loo! Unakaa kwenye hoteli ghali sana Lulu, lazima baba yako awe tajiri sana."



"Hata, baba yangu ameisha kufa, na mama yangu pia."



"Huenda hata baba yako alikuwa tajiri sana, kuwa amekuachia mali nyingi sana. Na huenda kaka zako matajiri sana."



"Kaka yangu alikuwa mmoja tu, lakini alikufa huko Kampala kwa bahati mbaya baada ya kupigwa risasi wakati wa msukosuko kati ya Serikali na Kabaka. Halikuwa kosa la askari maana yeye mwenyewe ndiye alikuwa akizagaa mjini. Sasa niko peke yangu, na baba yangu hakuwa tajiri ila alikuwa anakijishamba kidogo cha kahawa tu, karibu na Kampala.



Tuseme maonyesho ya mavazi ndiyo yanayokuhifadhi kiasi hiki, eti?"



Aah Joe, unataka kuingilia katika maisha yangu? Nadhani ulikuwa ukija kunipa heko kama ulivyosema, lakini inaonekana sivyo. Nadhani utanibusu ukinipongeza!" Alisema kwa sauti ya mshangao sana.



Alisogea karibu yangu akanivuta. Akafungua tai yangu akaingiza mkono wake ndani ya shati langu na kisha akanibusu.



"Nimekupenda sana Joe, tangu nilipokuona siku ya kwanza katika Starlight Klabu. Oh! Sijui kwa nini sikuweza kukuona mapema."



"Kwani sasa unaye mpenzi wa kukuzuia usinipende?"



"Ndiyo nimeisha mpata, na naona siwezi kumwacha," alijibu huku akionyesha huzuni.



"Ni nani huyo?"



"Benny, yule niliyemfahamisha kwenye maonyesho."



"Tangu lini mmeanza mapenzi?"



"Tangu jana."



"Jana! Usinieleze, jana tu mmeisha ahidiana kuoana?"



"Kwani ni ajabu?"



"Mlikuwa mnafahamiana zamani?"



"Ndiyo, nilipokuwa nikija huku mara kwa mara alikuwa akinichukua katika gari lake."



"Ndiye amekupangisha katika hoteli hii naona."



"Ndiyo, Benny ana fedha si mchezo."



Kwa muda sote tukawa kimya. Kisha nikafumbua midomo,

"Samahani Lulu, ninasikitika kuwa nina jambo la kukuuliza," nilisema taratibu huku moyo wangu ukipiga upesi, maana hata mimi sikupenda kumchukiza msichana Lulu.



"Uliza tu Joe."



"Kwa nini katika maonyesho ukiwa kwenye jukwaa kunatokea mauaji wakati huo huo?"



Aligeuka rangi, nywele zikamsimama. Alikuwa anafunguwa vifungo vya shati langu, akaacha. Alikuwa akinibusu, akaacha! Na hapo hapo midomo yake yenye joto ikiwa baridi. Kisha akajibu " Mimi sijui, maana huwa niko kwenye jukwaa."

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Mbona leo wamekubadilisha zamu yako na kutoka mapema? Na ulipotoka tu yakatokea mauaji, hasa wakati watu wakikushangilia?"



"Wewe ni nani mpaka uulize mambo kama hayo? Wewe si Polisi, waachie Polisi, waje wauulize. Sitaki maswali kama hayo. Na kama ndiyo yaliyokuleta humu toka kabla hujajisikitikia kwa nini unauliza maswali kama hayo."



"Sisi waandishi wa habari ni wazungumzaji wa mambo mengi kwa hiyo usijali. Kama hupendi hilo swali sasa nikueleze jambo jingine."



"Jambo gani," alisema huku macho yake yakionyesha hofu tupu.



"Kabla ya maonyesho hayajaanza Benny alikuwa akizungumza na wewe. Na akakueleza kuwa wanataka kuwaua watu fulani fulani. Kwa hiyo wewe utaambiwa uende kwenye jukwaa baada ya zamu kubadilishwa na James, Kijana wa kwenye jukwaa ambaye angepata ishara toka kwake. Kisha wewe utatoka kwenye jukwaa na kuwatia watu moto kwa mikogo yako ya ajabu. Halafu wao watapata muda kwa kuua bila kutambuliwa."



Alianza kutetemeka baada ya kusikia mambo hayo,"Mbwa wa Kishenzi we, nani alikuambia mambo hayo yote? Na kwa nini, unaingilia mambo yasiyokuhusu. Toka humu kabla hujawa maiti." Aliposimama alikuwa ameisha toa bastola iliyofichwa katika gauni lake kifuani, chini ya matiti.



"Toka, toka nje ya chumba changu la sivyo utakufa. Pilipili usiyokula inakuwashia nini?"



Nilimjibu huku nikicheka, "Wasichana wazuri kama wewe, hawafai kuwa na bastola, hebu iweke bibie, huenda tutazungumza vizuri kidogo."



"Unadhani natania, nakuua sasa." Kabla hajafyatua bastola yake, nilikuwa nimeishashika mkono wake. Nikaupinduapindua vizuri sana. Nikaichukua bastola yake na kuiweka ndani ya mfuko wangu wa koti.



"Mama Joe aliniambia usiwadhuru wasichana wazuri bure. Sasa nieleze uhusiano wako na mauaji haya. Na kama hutasema, miye nina ushaidi kamili wa kuweza kukupeleka mahakamani na ukahukumiwa kutiwa kitanzi."



Mlango ulifunguliwa na Benny akaingia pamoja na vijana wengine wanne, wote walikuwa wameshikilia bastola mkononi. Lulu alikimbia mpaka kifuani kwa Benny.



"Aha, mpenzi naona umeniletea zawadi nzuri sana, maana nilikuwa nimejaribu kuipata nimeshindwa." "Ahsante sana Lulu mpenzi."



"Wananchi waheshimiwa wenzangu, nadhani hamtastaajabu nikiwafahamisha kwa Willy Gamba, Mpelelezi maarufu sana katika Afrika hii. Anafanya kazi katika Idara ya Uchunguzi Tanzania. Naamini kila mtu anamjua kufuatana na usomaji wa habari zake katika magazeti ingawaje si kwa sura. Leo tunafurahi kuwa ndani ya mikono yetu na tunaweza kumfanyia lolote lile."



Alipokuwa akitoa hii hotuba yake fupi, niliona rangi za wengine wote zimebadilika sana hasa ya Lulu, na walionyesha mshangao mkubwa sana.



"Willy, ulikuwa mjinga sana ulipodhani umetufunika kwa kutumia jina la Joe Masanja kwamba ungeweza kutupumbaza! Lakini ujue kuwa kundi letu ni kubwa. Na lina watu wa aina nyingi na hata watu wenye vyeo vikubwa sana serikalini . Kwa vile kupata habari za aina yoyote ni rahisi sana. Hata John alipokuja hapa alijifunika kwa jina la Fred, tulijua mapema zaidi ya tulivyokufahamu wewe."



"Kwa nini ulimwua John?" Nilimwuliza.



"Kwa sababu alikuja kuingilia mipango yetu, jambo hata wewe hilo hilo muda si mrefu."



"Nilicheka hapo kidogo halafu nikamweleza, "Unadhani unaweza kusalimika na tendo hilo? Unajidanganya sana Benny. Ninakusikitikia kijana kama wewe kufa katika umri mdogo kama huu."



"Si mara yangu ya kwanza kufanya jambo kama hili, na nina akili zaidi yako na fedha zaidi ya kila mtu hapa Afrika ya Mashariki hasa itakapofika kesho kutwa nitakuwa na maelfu ya fedha. Na unajua kila siku fedha zinaweza kuponyesha mtu, kwa hivyo sitadhurika hata chembe. Najua nikiisha kukuua wewe sasa hakutakuwa na kizuizi katika mipango yangu," alisema kwa dharau sana.



"Hizo karatasi ziko wapi Benny?" Niliuliza.



"Hilo siwezi kukuambia, maana hata hawa wengine hawajui zilipo ila mimi tu."



"Lakini jua kuwa ukiniua mimi hapa, Lulu atashikwa sasa hivi maana watu wote wanajua niko hapa kwake," nilimwambia nilipotazama saa yangu na kuona karibu saa nne u nusu Sammy anipigie simu.



"Eh, unadhani miye ni mtoto katika kazi hii! Huwezi kunidanganya kwa jambo hili hata kidogo, maana hata mimi nimewahi kutishia watu na uongo wa namna hiyo !"



Alipotaka kuendelea kusema simu ililia, Lulu alienda kuijibu. Kisha aligeuka na kusema kuwa ilikuwa simu yangu. Benny alionyesha kuchukia kabla ya kusema, "Haya kaijibu tusikie utaongopa nini, mbwa we."



"Hallo, huyu ni Willy," nilijibu. "Oh, fanya hivi, kama usiponiona kwenye dakika tano hivi hapo basi, piga simu polisi uwajulishe habari yangu, na kwamba waje mpaka katika hiki chumba," niliendelea kusema.



"Ndiyo ndiyo, kumbe wengine wapo hapo chini, haya waambie hivyo. Asante sana kwa heri mpaka tutakapoonana kwenye dakika tano hivi," nilimaliza.



Wakati nikijibu simu, Benny, Lulu na wenziwe walionekana wamechukia sana. Tangu walipoingia wale vijana wanne walikuwa wameshikilia bastola zao tayari kufyatua baada ya kuamriwa tu na Benny. "Unasemaje mpenzi Benny, utaniua ama unaniachia huru niende zangu? Maana ukiniua tu utashikwa mara moja, kumbe hata polisi wengine wako nje ya hii hoteli," nilisema huku nikisimama taratibu kabisa.



"Oh, tutaonana siku nyingine Benny, na siku hiyo tutakapoonana si kama ambavyo tumeonana kirafiki hivi," Ilionekana hawakuwa na njia ila kuniachilia huru tu.



"Na wewe Lulu, siku nitakapokupata nitakupa siafu kwenye hayo mapaja yako wayaumeume, kusudi uweze kujikuna ovyo hata mbele ya baba mkwe wako,"



"Huwezi kuudhi mwanamke namna hiyo, na nitahakikisha kuwa unakufa kabla ya kesho jioni," alisema Lulu huku chuki imemjaa.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Alamsiki nyiye wote, niliondoka na kufunga mlango nyuma yangu.





Nilitelemka taratibu kabisa mpaka chini. Hapo chini sikumkuta mtu yeyote, licha ya Sammy niliyetegemea kumuona. Niliingia katika gari yangu mpaka hotelini kwa Sammy. Nilimkuta Sammy akisoma gazeti liitwalo. 'The Detective' nilimweleza mambo yote niliyoyapata kutoka kwa Lulu



Sasa tulianza kuelewa mambo yote yalivyo, "Inaonekana Lulu ameingizwa katika mpango huu kusudi amsaidie Benny katika mambo fulani fulani. Mojawapo likiwa kama yale aliyokuwa akiyafanya maonyeshoni. Laiti isingekuwa sababu kama hiyo basi Benny asingefanya mapenzi na kupoteza fedha nyingi kwa Lulu. Pia tulianza kutambua kuwa Benny siye 'Bosi' ila 'Bosi' mwenyewe yupo', na Benny ndiye msaidizi wake.



Hivyo zile karatasi anazo 'Boss'. Na anayemjua huyo 'bosi' ni Benny peke yake wengine wanadhani 'Bosi' ni Benny.



Kwa hiyo kazi kubwa sasa ni kutafuta kwa kila njia tumjue huyo 'bosi' ni nani. Na kwa kufuatana na habari nilizozipata kwa James, hizo karatasi zitabadilishwa kesho usiku.



Jambo jingine ambalo lazima tuchunguze ni mahali ambapo mabadilishano ya karatasi hizo yangefanyika. Kwa kuwa wamekwishajua kuwa tunafanya kazi juu ya jambo hili, wanaweza wakaharakisha mambo zaidi na wakazibadilisha hizo karatasi haraka iwezekanavyo. Kwa hiyo nasi inatubidi tufanye kazi haraka kusudi tuweze kuzipata hizo karatasi kabla ya wao kuwapa hao watu, na kabla hawajalipwa.



Haya ndiyo mawzo yangu niliyokuwa nayo. Sammy pia alionekana kuwa na mawazo kama hayo. Tulimpigia Robin simu, tulimweleza juu ya mambo yote tuliyokuwa tunafikiri. Robin alisema, "Ninaona mawazo yenu ni sawa. Walakini inafaa mnipe wasaa maana mimi na vijana wangu tunaanza kupata fununu ya jambo fulani."



Sammy alitoa wazo kuwa yeye ataenda kuchunguza katika ile nyumba ya Benny kama anaweza kupata habari yeyote, kusudi mimi anipe nafasi nilale. Lakini mimi sikukubaliana naye niliona miye ndiye niende, na yeye akiona sirudi, anaweza kuja kunitazama huko. Maana kila siku tunapokuwa tukifanya kazi na Sammy, miye huenda kwanza tukijua ni mahala penye hatari na yeye huja nyuma. Na mara nyingi hii imefanya kuokoa maisha yetu.



Sammy alisisitiza kuwa, kwenda kule peke yangu kunaweza kuwa na maana ya kifo, kwa hiyo ni afadhali twende sote pamoja. Lakini bado niliona hili si sahihi. Mwishowe alikubaliana nami kuwa mimi niende kwanza halafu yeye aje baadaye,baada ya muda kama wa saa moja hivi.



Nilirudi hotelini kwangu nikabadilisha nguo. Mara hii nilichukua bastola mbili, moja ile yangu ya kawaida, '45 automatic' na ya pili ndogo kiasi cha kalamu ya wino. Hii ya pili niliisukuma kwenye mkunjo wa chupi niliyovaa.



Halafu nikanywa bilauli moja ya maji na whisky. Kisha nikaandika kijikaratasi cha kumwachia Lina, maana nilikuwa namtegemea usiku ule saa sita. Alikuwa amenipigia simu kuwa huenda angalikuwa na jambo kamili ambalo lingeliweza kunisaidia, wakati huo. Ghafla nikajiwa na wazo nimpigie Lina simu, nimweleze kuwa sintokuwepo ila nitaenda kufanya uchunguzi kwenye nyumba ya Benny.



Hii ingenisaidia mambo fulani fulani. Kwanza kama nikimpigia simu Lina, na kama Lina ananicheza yuko upande wa Benyy nitakuta Benny yuko tayari ananingojea maana Lina atamweleza hizi habari. Pili Lina amewahi kuwa mpenzi wa Benny kwa hiyo anafahamu kila kona ya kile chumba. Kwa hiyo anaweza kunipa muhtasari wa jinsi nyumba ilivyojengwa na jinsi vyumba vilivyokaa na hakuna uwezekano wa kufichwa vitu vya siri. Mwanamke..... japo siku moja tu ukikaa naye atakuwa amejua wapi hutaki aende na wapi unataka aende. Basi nilimpigia simu Lina.



"Hallo huyu ni Willy, habari Lina?"



"Salama tu Willy, mbona unanipigia simu na hali nimekwambia nitakuja? maana mpaka sasa nangojea simu toka mahali fulani ambayo inaweza kukusaidia sana."



"Oh. unafanya kazi vizuri kabisa Lina. Sababu ya kukupigia simu ni kwamba ninatoka. Naenda kufanya uchunguzi kwenye nyumba ya Benny, kwa hivyo nilitaka unipe muhtasari wa nyumba ilivyokaa, na jinsi ninavyoweza kuingia ndani kwa usalama bila kuzuiliwa."



"Lakini Willy, maahala hapo ni pa hatari sana. Mimi nilipopita karibu na mahali hapo niliona baada ya kuchunguza sana kuwa pamejaa walinzi. Na wote wako tayari kuua mtu yeyote atakayeenda hapo. Miye nilifanya uchunguzi huo nilikuwa huko 'Sclaters hosteli' na niliambiwa hivyo na msichana fulani ambaye ni shemeji ya Benny. Aliniambia kuwa Benny alikuwa amemwambia asiende pale leo maana pana hatari. Na kuwa ingekuwa salama kwake kama angebaki hostelini. Kwa hivyo mimi naona usiende, utahatarisha maisha yako bure tu, tafadhali."



"Hapana Lina, lazima niende. Na wewe njoo kwenye chumba changu ifikapo saa sita hivi. Nadhani bado una ufunguo niliokupa. Wakati huo nina uhakika kuwa nitakuwa nimerudi. Na kama nitakuwa sijarudi jua basi kumetendeka jambo. Sasa nipe huo muhtasari basi."



"Sikiliza Willy, nyumba yenyewe ina vyumba vitano sebule ya sita; choo, bafu na jiko. Vyumba vya kulala vine. Kile cha sita ni namna ya maktaba, maana huwa mna vitabu vingi sana na wageni hawaruhusiwi kuingia humo maana ndipo anatunzia bastola zake na hata za rafiki zake. Nyumba hiyo ina milango mitatu ya nje. Mmoja nyuma kutokea kwa 'Nakuru road'. Upande usio na mlango ni ule wa kulia, ambao unapakana na 'Scrates hosteli,' ila una dirisha moja kubwa la kutosha mtu kuingia kwa dirishani.



Unapoingia utaangukia ndani, utakuwa katika chumba kimoja cha kulala lakini hakina mtu sasa, maana yule shemeji yake ndiye alikuwa akilala humo. Vyumba vyote vya nyuma ni vya kulala. Benny analala kwenye chumba kinachofuata hicho chenye dirisha, mkono wa kushoto wa hicho. Chumba kinachotazamana na mlango wa mbele ukiwa sebuleni, ndicho hicho nilichokueleza, kinachotumiwa kama maktaba. Unataka nikueleze nini tena mpenzi!"



"Hayo yanatosha Lina, asante sana. Kama nikirudi salama ndipo nitaweza kutoa shukrani kwa udhati mbele yako. Hapana shaka tutaonana. Kwa heri mpaka hapo." nilijitengeneza sawasawa, mara hii nilionekana kama mpelelezi haswa mwenye cheti cha kuua.



Nilitoka nje nikaingia ndani ya gari yangu, nikaelekea Westlands. Nilipokuwa ninaenda niliona gari kama mbili zinanifuata kila ninapopita. Nilipofika karibu na 'Klabu 1900' nilisimama. Hizo gari mbili zilikuja zikanipita. Nilipoangalia nikagundua kuwa katika gari la mbele mlikuwa na vijana wawili ambao niliwaacha chumbani kwa Lulu na Benny. Katika gari la nyuma mlikuwa na yule kijana niliyemrudisha wakati akitufuata nilipokuwa na Lina katika gari lake. Nao walienda wakasimama mbele yangu.



Niliwasha gari langu moto nikaenda kulisimamisha na magari mengine hapo klabu 1900. Halafu nikangoja, wale jamaa nao wakaja wakasimamisha magari yao hapo nje kisha wote wakatoka na kuingia klabu 1900. Walidhani mimi nimetoka na kuingia humo, maana nilipokuwa nikizimisha gari langu kijana mmoja naye ndiyo kwanza anawasili hapo, alitoka katika gari lake na kuingia ndani. Alikuwa amevaa koti kama langu, na ni mrefu kama mimi, kwa hiyo walidhani ni mimi. Kisha nilitoka katika gari langu, nikaenda kwenye magari yao, nikapiga risasi magurudumu yote manne ya kila gari, yakawa hayana kazi alafu nikaenda katika hiyo klabu ambamo niliwakuta wote watatu wamekaa huku wakiangaza macho huku na huku. Nilienda nikakaa kwenye meza moja nao alafu nikawaambia,"Tafadhalini wazee, mimi sitaki kufuatwa fuatwa, na kama mkizidi mtaona cha mtema kuni. Mimi nilikuwa nikija hapa kunywa na nyie mnanifuata tu. Sasa nitawaacha hapa, na ninarudi kunywa mjini, na yeyote atakayenifuata nitamwadhiri vibaya sana." kabla hawajajibu niliondoka na kurudi kwenye gari langu. Nililitia moto na kuondoka halafu nikaenda kusimama hatua chache nione kama watatoka.



Kitambo walitoka, na kuingia katika gari zao. Walipowasha wakakuta magurudumu hayana upepo yote. Walitoka na kuanza kuzungumza. Miye Willy nikaweka gari langu moto, kuendelea na safari yangu.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Niliondoka hapo kwa mwendo mkali mno. Nilipofika kwenye ile nyumba nikapunguza mwendo. Nikasimamisha gari mbele ya Sclaters hosteli karibu na miti. Hlafu nilianza kurudi kwa miguu, taratibu. Nilikuwa nimeacha koti langu katika gari, halafu nikavaa kijambakoti, ambacho kinanifanya mwepesi zaidi.



Nilienda nikavuka Sclaters hosteli kisha nikaangaza macho yangu mbele ya nyumba hiyo nikaona watu wawili wakizungukazunguka hapo mbele. nikaenda kuchungulia upande wa nyuma pia nikaona kuna walinzi, kama Lina alivyosema. Nyumba yote ilikuwa giza maana hamkuwa na mwangaza hata sebleni. Basi nilikata shauri nifanye kama Lina alivyosema Hapo nikaanza kumsifia Lina kwamba yu mwenye akili hasa. Na kwamba angefaa sana kufanywa mpelelezi.



Nilienda nikaruka seng'enge, nikawa nimeisha anguka ndani ya seng'enge. Lakini mmoja wao alisikia namna ya kishindo kwa hiyo akaja upande ule wangu. Nilijibanza kwenye ukuta. Aliposogea karibu nikamtupia kisu shingoni. Hatimaye mtu huyo alikufa bila mtu kujua.



Nilipanda mara moja kwenye ukuta, nikakwea taratibu bila kufanya kelele yeyote, mpaka nikashika kwenye dirisha. Hlafu nikatoa tochi yangu na kumulika ndani ya chumba. Nikaona kulikuwa kumelala mtu kwenye kitanda huku ameshikilia bastola mkononi alikuwa amesinzia. Alionekana kana kwamba anataka kuamka lakini kabla ajaamka nilimtia kisu shingoni pia. Akawa hoi bila kutoa sauti. nikaanguka kwenye kitanda bila sauti kutoka kwenye dirisha.



Mlango wa hicho chumba ulikuwa umefunguliwa, kwa hiyo nilitoka nje ya chumba hicho bila kufanya kelele hata kidogo. Nilijaribu mlango wa pili yake ambao Lina alisema ndimo Benny alikuwa akilala, nikakuta umefungwa. Nilichukua funguo yangu malaya nikafungua, nilipopiga tochi mle ndani nikakuta hakuwemo mtu. nilienda kwenye kimeza cha karibu na kitanda, nikaanza kutafutatafuta vijikaratasi vyovyote vya maana lakini sikuona. Ila nilipata karatasi moja ya simu imeandikwa kwa kimombo. 'TELL THE BOSS TO MAKE SURE IT WON'T BE LATER THAN TUESDAY AT 10:00 P.M BECAUSE WE ARE EXPECTING THEM TO LEAVE THAT NIGHT AND BE HERE THE NEXT MORNING.' Fasili yake kwa kiswahili 'umwambie 'BosI' kuhakikisha kuwa Haitazidi jumanne saa nne usiku, maana tunawategemea kuondoka usiku huo na wawe hapa asubuhi ifuatayo"



Nilitoka kwenye hicho chumba na kufungua mlango nyuma yangu kisha nikaharakisha kwenda sebleni, kutafuta mlango wa maktaba. Maana nilikuwa nafikiRi kama Lina alikuwa anasema kweli, basi huenda humo ndimo mngepatikana mengi.



Niliingia sebuleni, bahati mbaya nikajigonga kwenye kiti: Yule kijana aliyekuwa mbele ya nyumba alishtuka. Niliweza kumuona sababu mlango ulikuwa wa vioo. Alikaa kidogo huku anaangaza macho ndani, nadhani kwamba alifikiri alikuwa yule mwenzake aliyekuwa amelala mle chumbani, lakini mwishowe alikata shauri ahakikishe, kwa hiyo alifungua mlango.



Mimi nilijibanza kwenye ukuta, alipoingia na kutaka kuwasha taa, nilimmulika na tochi machoni na hapo hapo nikatupa kisu, kikapambana naye kifuani. Kumbe na yeye alikuwa amefyatua bastola yake, na wakati alipoanguka tu, bastola yake ikafyatuka na kutoa sauti.



Wale walinzi wawili wa nyuma, walikimbia kwenye mlango wa mbele. Miye nilikuwa tayari nimekwishajibanza na bastola yangu nikiwangoja. Nilisimama kwenye 'swichi' ya taa kusudi wasije wakawahi kuwasha taa. Walipoangalia nje bila kuona lolote, walifungua mlango na kuingia ndani. Mmoja aliyekuwa mbele alitaka kuwasha taa hapo hapo nikaziachia risasi. Bastola yangu ilikuwa na kiwambo kwa hiyo haikutoa sauti. Yule wa nyuma akiwa bado anashangaa pia alizipata risasi.



Mara hii sikuwa na mchezo, madhihaka yote yalikuwa yamekwisha. Nilikuwa nimeishawachukia hawa watu kama kufa, hasa kwa sababu ya mauaji ya John. Kwa hiyo hata mimi sikuwa na huruma hata kidogo. Inaonekana kulikuwa na walinzi kama watano hivi na wote nilikuwa nimewafyeka kabisa.



Nilipiga tochi yangu sebleni, alafu nikakimbia kwenye mlango wa maktaba nikafungua na funguo zangu malaya. Nikaingia ndani halafu nikajifungia na kuanza kupekuapekua. Mlikuwa na vitabu vingi sana. Mlikuwa na masanduku ya vyuma yote yakiwa yamejaa vitabu. Nilifungua kabati moja la chuma, nikaona mlikuwa na bastola kadhaa pamoja na risasi. Pia niliona bahasha moja ambayo ndani yake mlikuwa na barua. Juu yake ilikuwa imeandikwa Dr. Dickisoni Njoroge.



Nikiwa bado naendelea na upekuzi wangu bila kufanikiwa kupata chochote nilichokuwa nikikitaka, nilisikia mlango wa maktana unafunguliwa. Zilikuwa zimepita dakika kumi. Na nilikuwa nimeweka dakika kumi na tano tu kuwa kwenye nyumba hiyo, kwa hivi zilikuwa zimebaki dakika tano. Na Benny alikuwa ameisha niwahi kabla sijaondoka.



Nilijificha nyuma ya kabati hilo la chuma. Alipofungua aliwasha taa, hakuwa Benny ila kijana mwingine. Aliangaza huku na huko bila kuniona. Lakini mwishowe niliona akija upande wangu. Nilitoa kisu changu, kabla hajageuka, nikampata mgongoni, akaanguka bila hata yowe! Nilikimbia mlangoni. Nikaangaza sebuleni ambamo sasa taa zilikuwa. Sikuona mtu, nikakimbia mpaka kwenye mlango wa mbele, kabla sijatoka nje, nilipigwa kichwani mpaka chini.



Nilipozinduka nilijikuta nimefungwa kitini! Karibu yangu alikuwa Sammy pia amefungiwa kitini huku bado amezimia! Benny na Lulu walikuwa wamesimama karibu nami huku wakionekana na furaha sana.



"Naamini muda huu huna ujanja Willy, ninakuhurumia sana, maana kifo chako pamoja na rafiki yako kitakuwa kibaya na cha maumivu sana. Nami nitahakikisha kuwa mmekufa kwa taabu maana nyie mnaonekana watu wa ajabu sana, kumbe mambo yote waliyoandika juu yako ni kweli".



"Wewe umeniingiza hasara sana ya watu wangu, maana umeua sita, na huyu rafiki yako ameua watano wakati akijaribu kuja kukuokoa lakini na yeye ameangukia kwenye mkasa huo huo." Alisema kwa kujivuna sana.



"Sasa unadhani utafaulu kwenye mipango yako eti?"



"Kwanini nisifaulu, mpaka sasa yote yamekwisha kamilika, ila wewe tu na huyu rafiki yako ndiyo mlikuwa mnanipa taabu, lakini sasa hamtanipa taabu tena. Na sasa watu wangu wote watafanya sikukuu wakisikia wewe, John, na huyu anayeitwa Sammy amekufa".



"Umefahamje kuwa huyu ni Sammy?"



"Lo! Wewe ndiye umechelewa kweli, nimekwambia saa zile kuwa kikundi chetu hata polisi wenyewe wamo. Nitashindwaje kujua basi. Nyie kila siku mnadhani ndiye wenye kujua habari nyingi, lakini mimi nina habari nyingi zaidi yenu, na ninatumia akili zangu zaidi yenu nyie. Na pia nahakikisha kuwa sifanyi kosa hata moja".



"Hii mipango mmeianza lini, na nani aliwasaidia katika jambo hili maana nyinyi msingelijua wapi pa uhakika ziliwekwa hizo karatasi?"



"Bosi' aliniambia kwamba nisiwaeleze jambo lolote mpaka amri itakapotoka kwake, lakini kwa sababu miye sitaki kuwaona mnaishi tena, nimeleta madebe mawili ya 'Petrol' na vijana wangu watawamwagia na kuwawasha moto mpaka mtakapokuwa mmeungua na kubaki majivu."



"Unafurahi, kuchoma watu eh Benny, lakini kabla sijamalizika kabisa wakati nikiungua na wewe utakuwa umekufa." Nilijibu kwa dhihaka.



"Uh, unadhani natania, Amani. Lete hayo madebe ya 'Petrol' pamoja na kiberiti," aliita kwa hasira.





Wakati huo Sammy alikuwa ameisha zinduka akasema, "Wewe shetani mwanamke, siku moja nitakata kipande cha nyama katika mwili wako na kukifanyia sikukuu."



"Nyamaza mwehu we, utaikataja nyama yangu na hali utakuwa umeisha kufa?" Alisema huku akitabasamu.



"Naona hapa tutakufa kama wanawake Willy, lakini hata hivyo huyu mwehu atashikwa na kutiwa ndani, nitafurahi sana kumpokea huko chini, na lazima nitahakikisha kuwa atapata taabu mpaka kupata makao," alisema Sammy huku akionekana hajali lolote. Benny alitoa kicheko. Halafu akamwambia Aman atumwagie petrol.



Kabla hajamwaga Lulu alitoa oni, "Nadhani 'Bosi' atapenda kuwaona hawa washenzi wakiungua, kwa hiyo afadhali tumfuate aje ajionee hawa watu mashuhuri wa Serikali wakifa kitoto, na kifo cha aibu. Unaonaje Benny?"

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Lakini lazima tuache ulinzi wa kutosha hasa. Mlango wa nyuma weka walinzi watatu. Huu wa mbele watatu. Na wengine kuzunguka nyumba, halafu kwenye mlango wa chumba hiki watatu pia. Naamini hata kama angekuwa malaika hawezi kutoroka kwenye ulinzi wa namna hii."



Wazo wako ni zuri sana Lulu. Nadhani 'Bosi' atafurahi ajabu na atatufanyia sikukuu. Lakini nyie wote angalieni kuwa hamfanyi kosa hata kidogo. Kosa lolote mshahara wake ni kifo cha namna hii hii.



Nilimuuliza mlinzi mmoja aliyekuwa akifunga mlango wa chumba tulichokuwa, "Itawachukua muda gani kwenda kwa 'Bosi' na kurudi?"



"Kama dakika kumi hivi". alijibu na kisha akatufungia ndani. Halafu wakasimama pale mlangoni hali walinzi watatu wakiwa tayari na silaha zao.



Tulikuwa tumefungwa sana, hivyo kwamba hatukuweza hata kujitingisha. Walikuwa wametuvua nguo zetu zote isipokuwa chupi tu ajabu ni kwamba niliweza kusikia bado bastola yangu ndogo imo kwenye mikunjo ya chupi yangu. Jinsi ya kuitumia ilikuwa haifahamiki hata kidogo. Kuwa nayo na kutokuwa nayo yote yalikuwa mamoja. Na pia tulijua tungefanya upuuzi wowote kabla Benbny, Lulu na 'Bosi' hawajarudi tungeliteswa na hawa walinzi.



"Mara hii hatuna ujanja kweli Sammy."



"Hata mimi naona, maana sidhani kwamba kunaweza kuja mtu wa kutuokoa, na kama pia atakuja atakufa kabla hajafika humu ndani!"



"Mie nilikuwa siku zote natabiri kufa kwa risasi, maana pia nimeisha ua wengi kwa risasi".



"Hakuna njia Willy, ila huenda mizimu ya mama Sammy ifanye kazi yake. Unakumbuka tulivyopona safari ile kule Lusaka?"



"Ndiyo, nakumbuka, lakini ulinzi pale haukuwa mkali kama huu wa hapa".



Mawazo yangu yalirudi Dar es Salaam. Nilimfikiria mpenzi Della, moyo ukaniuma namna ya ajabu. Nilijua Della angeweza kujiua kama angesikia nimekufa. Nilimpenda naye alinipenda. Alikuwa msichana wa peke yake aliyechukua moyo wangu na ambaye nilichukua moyo wake. Kisha nikamfikiria mama Willy. Lo! Mimi nilikuwa mtoto wake wa pekee. Hakuwa na mtoto mwingine hata mmoja. Mama Willy nilijua atakapoambiwa tu, ataanguka chini na kufa. Nilijua jinsi mama alivyokuwa akinipenda.



Nilionekana kama mawazo yangu si sawa. Nilikuwa katibu nipate kichaa kwa kufikiri mambo kama haya. Kisha nilimsikia Sammy akisema, "Nimesikia kitu kama mlio wa bastola yenye kiwambo!.



"Unaota nini Sammy".



"Hapana, kweli nimesikia." Kisha nami nilisikia kishindo kwenye mlango kana kwamba watu wanaanguka.



Mwishowe nilimwambia Sammy kuwa huenda ni 'Bosi' anafika kwa hiyo watu wanamtolea njia.



Tulisikia mlango wa chumba ukifunguliwa. Moyo wangu uliruka kwani nilijua sasa mwisho wetu umefika. Maana "Bosi" amafika. Nilipomtaza Sammy niliona nywele zake zikisimama na rangi ilibadilika. "Wameisharudi! Alisema.



Mlango ulipofunguliwa tulishtuka kuona ni Lina ndiye anafungua mlango. Alikuwa ameshika bastola mbili mkononi. Akazitupa chini akaja kunifungua. "Harakisheni tutoke hapa mapema kabla hawajarudi, maana nasikia watarudi mnamo dakika mbili au moja unusu hivi."



Mauaji ya kikatili



Baada ya kunifungua mimi, nikavaa upesi upesi, kisha nikachukua bastola moja, nikaenda kulinda mlango wa hiki chumba wakati Lina akimfungua Sammy. Sammy alivaa upesi upesi, nikamtupia bastola moja, na nikamtupia Linna nyingine, mie nikatoa bastola yangu ndogo kwenye mkunjo wa chupi yangu.



Nilifungulia madebe ya petroli halafu, nikayawasha moto, tukakimbia kutoka humo ndani. Tulipofika kwenye mlango, tulikuta walinzi wa nje tayari wamefika. Lakini hawakutuweza maana wote tulikuwa tunafahamu hasa namna ya kutumia bastola, tuliwaua wote. Tulikimbia mpaka kwenye gari la Lina, tukaingia ndani, Lina akaweka moto tukapaa zetu. Tulipokuwa tunaondoka tuliona gari la Benny, Lulu na 'bosi' likiingia. Fikiria kitisho walichokikuta humo ndani!



"Turudi tukawagutue Willy, nadhani tunaweza tukawakamata vizuri sana wakati huu, maana hofu zitakuwa zimewajaa," alisema Sammy.



"Achana nao Sammy. Kama tukiwashika sasa siri nyingine hatutazipata maana miye nataka tulifutilie mbali kundi, lote la wahaini."



"Asante sana Lina, sijui nitakupa nini kwa kuponyesha maisha yetu. Shukrani nilizonazo Maurana ndiye ajuaye. Sikutegemea kama ungeweza kufanya jambo la ajabu kama hili, maana nadhani hata mimi mwenyewe ningeshindwa kufanya jambo lolote kama ulilolifanya." Nilimshukuru Lina. Kusema kweli nilikuwa namwangalia Lina kama Malaika aliyetumwa kutoka mbinguni kuja kutuokoa. Usiku huu alionekana mzuri kuzidi wanawake wote niliokwisha kuwaona. Kila kiungo changu kilimpenda hata kucha zangu zilimpenda.



"Ulijuaje tuko hatarini Lina? Na ulijuaje jambo hili maana mpaka sasa mimi naona kama muujiza tu, hata siziamini akili zangu." Sammy alimuuliza.



"Nitawaeleza lakini sasa si wakati mzuri, maana Benny anaweza akatufuata, kwa hiyo ngoja mpaka tufike hotelini kwa Willy, kwanza." alijibu Lina huku amekaza macho yake mbele ya barabara. Tulikuwa tunaenda maili mia kwa saa kwenye hii 'uhuru Highway'."



Tulienda mpaka hotelini kwangu Embassy, Lina alisimamisha gari lake mbali kidogo na hotelini, kisha akarudi tukaenda chumbani kwangu. Tulikuta kuna pombe, Lina alikuwa amenunua chupa nzima ya 'dry gin' alipokuwa amekuja kukutana nami wakati tuliosemezana. Lina alileta bilauli akaanza kutumiminia pombe. Tukaanza kunywa hali yeye anajilaza kwenye kitanda. Kama kaiwada yake wewe si msahaulifu nilikwambia kuwa msicha huyu hanywi pombe ila soda tu na 'baby-cham'.



Lina aliinuka akakaa kwenye kitanda. Kisha akasema. "Sammy ulikuwa na haja sana ya kujua jinsi nilivyofahamu na jinsi nilivyofauru. Willy alikuwa ameniambia tuonane hapa mnamo saa sita u nusu hivi. Miye nikaja hapa wakati huo, maana habari nilizokuwa natafuta nilikuwa nimeishapata kiasi. Nilingoja hapa kwa muda wa nusu saa! Willy alikuwa ameeleza kuwa ataenda kufanya uchunguzi kwenye nyumba ya Benny. Wasiwasi uliniijia nikahisi kuwa lazima Willy yupo taabuni, moyo wangu uliniuma sana kiasi cha kutovumilia, nikaona nimfuate na kama ni kufa tufe wote. Maana Sammy, nimekufa sana kwa Willy. Hilo kwa dhati nakiri.



"Basi nilikata shauri niondoke kwenda kwa Benny. Nilikuwa na bastola yangu, ambayo nilipewa na Benny enzi zake na mimi. Na nilikuwa ninaichezea kila siku hivyo kwamba hata mimi nina shabaha za kutosha. Nilipokagua humu ndani pia niliona imo pia bastola nyingine. na ilikuwa tayari imetiwa risasi, nikaichukua. Nilienda kule hotelini kwangu nikachukua ile bastola yangu nyingine ambayo pia ilikuwa imejaa risasi. Nadhani hamtastajaabu kusikia kuwa mimi naweza kutumia mikono yangu yote miwili barabara, hivyo nilikuwa na bastola mbili nikama watu wawili! Bastola yangu inacho kiwambo cha kupoteza sauti kama ilivyo ya Willy. Nyumba ya Benny ninaielewa sana na ulinzi wake pia ninauelewa. Nilijua lazima mara hii kuna ulinzi wa ajabu, lakini nilijua naweza kubahatisha, nikifa basi nitakuwa ninakufa kwa ajili ya mtu nimpendaye, kwa hiyo nitakuwa nimekufa kifo cha utu. Mtu niliyekuwa namuogopa ni Benny, maana najua ujasili wake akiwa na bastola.



Niliingia kwenye gari langu na kuondoka mpaka mbele ya 'Sclater hosteli'. Nilipoangaza nikaona gari la Willy. Niliposhuka na kulitazama nikakuta magurudumu yote hayana upepo hata kidogo. Hilo lilinipa uhakika kuwa Willy bado yumo ndani ya nyumba na yumo mswambeni. Niliendea nyumba ya Benny nilipofika kwenye wigo, niliona walinzi wengi wakiwa na silaha huku wakinong'onezana. Niliona nikiruka seng'enge nitaanguka ndani kwa kishindo kwa hiyo nikaona nitambae chini ya sang'enge.



"Kama unavyoniona mimi mwili wangu ni mwembamba kidogo. Basi nilitembelea tumbo kama nyoka, nikajivuta chini ya sang'enge nikatokea ndani, kwenye upande ule wa 'sclaters hosteli'. Nilijivuta hivi hivi mpaka kwenye ukuta. Niliposimama, bado hakuwako mtu aliyekuwa ameishaniona, hata yule mlinzi wa upande ule."



"Nilianza kujisogeza polepole mpaka kwenye pembe ya nyumba. Nilipoangalia niliona kuna walinzi wanne kwenye mlango wa nyuma. Kama ilivyo hii gauni yangu rangi yake usiku haionekani. Nikaona siwezi kuingia kwa mlango wa nyuma. Nikarudi kumvizia yule mlinzi wa upande wangu. Nikamtia risasi bila kuniona, nikajiona naweza kunyata harakaharaka kwenda upande wa mbele. Nilipofika kwenye pembe ya mbele nikawaona walinzi watatu. Walikuwa wakizungumza kwa sauti ndogo lakini iliyoniwezesha kusikia. Nilisikia mmoja wao akisema. 'Benny na Bosi'watarudi hapa dakika tatu hivi tangu sasa."



"Moyo wangu ulifurahi kusikia Benny hayupo. Kisha nilikohoa kidogo ili wale watu wa mlangoni waje pembeni yangu kuangalia kilikuwa kitu gani. Kweli wote walipumbazika na ujanja wangu, wote watatu wakaja.'Nia yangu ilikuwa waje ili niwauae bila ya wale wa ndani kujua kuwa wenzao wameishauawa.



"Nilikuwa tayari na bastola zangu, kabla hawajaniona nikawafyatulia, na wote wakaanguka bila ya wa ndani kutambua. Nilipochungulia kwenye kioo niliona kulikuwapo walinzi watatu, wote wameshikilia silaha huku wanatazama kwenye mlango. Nilijua tu, humo ndimo amefungiwa mpenzi wangu Willy. Hii ilinipa moyo na sikuwa na woga tena. Nilifungua mlango wa mbele taratibu kabisa, kabla ya wale walizi wa mlangoni hawajatambua.



"Niliingia sebleni bila kufanya kelele mpaka nikajibanza kwenye ukuta. Kisha nilijivuta taratibu kwenye ukuta na nilipokuwa mahali pazuri pa kuwalisha risasi na wao, mara moja nilijitokeza, na kabla hawajafanya lolote wote nikawaadhili. Ndipo hatimaye nikakimbilia kwenye ile jela yenu. Nikaokota ufunguo kutoka kwenye maiti ya mlinzi mmoja, nikafungua, ndipo nikawaoneni mkiwa mmefungwa pamoja na viti." alimalizia kutueleza Lina, huku akitoa tabasamu lenye huba na ukarimu.



Hatimaye Sammy alimuuliza Lina, "Jambo gani umelipata katika uchunguzi wako?"



"Kweli, karibu nisahau kusema. Sikupata mambo mengi sana ila tu kwamba ile nyumba ambamo Benny anakaa ni ya Daktari Dicksoni Njoroge, tajiri mmoja ambaye ana mashamba makubwa makubwa na ng'ombe wengi sana huko Thika na Nyeri, lakini ajabu ni kwamba Benny, halipi kodi ya nyumba, anakaa tu bure hali hawana ujamaa na Daktari Njoroge ndiyo hayo tu niliyopata sidhani kwamba yanaweza kuwasaidia kwenye mambo fulani." alijibu Lina huku akinitazama.



"Hizo habari zimenipa jambo na sasa lazima tufanye kazi upesi upesi. Nafikili huyu 'bosi' ndiye huyu daktari Dickisoni Njoroge, maana nilipokuwa nakagua katika kabati moja kwenye chumba cha maktaba, nilikuta bahasha imeandikwa 'Dr. Dickisoni Njoroge'. Na sasa nakumbuka ilikuwa na stemp za nchi ya ng'ambo. Na kufuatana na ripoti ya Lina inaonyesha kuwa lazima kuna uhusiano kati ya Benny na Njoroge. Lakini kabla ya kuanza kumfuata Njoroge inatubidi tuhakikishe kuwa ni yeye.



"Tusubiri tujue ni wapi Benny alikuwa akipiga simu alipokuwa kule 'City Hall' wakati wa maonyesho. Tutaulizia, kutoka polisi. Na wakati huu naona tukalale maana inaonekana saa zimekwenda sana, kwani kesho kazi zitakuwa nyingi sana!" Saa yangu ilionyesha saa tisa za usiku. Sammy aliondoka kwenda kulala, akatuacha miye na Lina hapo.



Lina aliniamsha alfajili yapata saa kumi na mbili na dakika arobaini hivi. Ilionekana msichana huyu ni kiumbe cha ajabu maana kichwa chake kinafanya kazi kama mpelelezi pia.



"Lina, mimi naona nitampigia Mkurugenzi wa Upelelezi Tanzania simu akupe kazi kwenye idara yetu maana utakuwa msaidizi mzuri sana kwangu na Sammy," nilimweleza Lina.



"Hapana Willy, mimi nataka tukitoka salama kwenye baa hili, na mimi nikiwa salama tuoane mara moja kabla ya wengine hawajakuzuzua."



Nilianza kuduawa nilipomuwaza mchumba wangu Della ambaye yupo nyumbani kwangu upanga. Na papo, uzuri wa Lina unanizubaisha. Nikamwambia, "Usijali Lina, lolote utakalo miye Willy nitatimiza, maana bila ya wewe mimi sasa hivi nisingekuwa Willy tu lakini jina langu lingeanziwa na 'Marehemu'......"



Kitambo nilipokuwa nikijitayarisha kwenda kuoga simu ililia. Nilipoenda kuijibu nilikuta Peter ndiye alinipigia simu."Unaendeleaje kijana, mambo yanaenda vizuri ama vipi maana ofisi yetu ya Dar es salaam wana wasiwasi mwingi sana, na wamenipigia simu asubuhi hii."



Nilimweleza Peter mambo yote yaliyokuwa yametupata mpaka muda huu, na jinsi tulivyofikiri mambo yetu yataendeleaje.



"Lakini unakaa wapi hapo Peter, ama umeishapata nyumba tayari?"



"Bado Willy, niko hapa 'New Stanley Hoteli' chumba nambari 101, kama ukitaka kuja kuniona." Peter alikata simu, miye na Lina tukaenda maliwatoni kuoga.



Tulipokuwa maliwatoni nilisikia simu ikilia, basi nilitoka huko na kuiendea simu.



"Halloo, Jeo huyu."

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Polisi Stesheni hapa."



"Eh mna ujumbe wangu wowote wazee?"



"Ndiyo, eh'



"Basi hii simu ilikuwa inapigwa huko Livingston Green, kwenye nyumba ya Dr. Dickison Njoroge."



"Asante sana bwana."



ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog