Search This Blog

Friday 18 November 2022

KUFA NA KUPONA - 5

 





    Simulizi : Kufa Na Kupona 
    Sehemu Ya Tano (5)




    Nilikata simu nikarudi maliwatoni kuoga. Kichwa changu kilijenga mawazo kutokana na taarifa hiyo ya Polisi kuhusu simu iliyopigwa.



    Baada ya kuoga, tuliletewa kahawa. Na baada ya hapo nikajitayarisha kwa ajili ya kazi za mchana. Nilipolisoma gazeti la 'East Afrikani Standard,' nilikuta taarifa kwamba maonyesho yangeanza saa mbili usiku. Lakini halikutaja zaidi habari za vifo vilivyokuwa vimetokea. Lina aliniambia alikuwa na hofu huenda Benny akafahamu kwamba yeye ndiye aliyetutorosha hivyo akaanza kumwinda. Lakini mimi nilimuhakikishia kuwa hatajua maana watu wake wote tulikuwa tumewahujumu, na watu waliokuwa wanajua ni Sammy na Peter ambaye nilimweleza tulipokuwa tukizungumza katika simu, na watu hawa hawawezi kumzuru.



    Sammy alifika hotelini kwangu mnamo saa mbili. Tuliamua kwenda kumuona Robin ambaye tulipanga kukutana saa kama hizo. Lina alisisitiza twende zetu naye kila mahali lakini siye hatukuonelea vizuri. Nilimtaka akae pale pale chumbani kwangu asiende kwake. Nilimwachia bastola moja ili kuitumia itakapobidi.



    Tuliondoka na kumwacha Lina mle ndani, tukaanza safari yetu kwenda New Evenue Hoteli ambako Robin alikuwa amepitia. Tulipofika kwenye ghorofa ya kwanza nikaamua kupiga simu Polisi ili kupatiwa vijana fulani fulani wakamvizie Dr. Dickison Njoroge waweze kujua myenendo yake ya siku nzima. Na lazima wawe wakipiga ripoti kwetu baada ya kila dakika 15 hivi kutujulisha myenendo hiyo. Na kama wakiona anafanya jambo fulani ambalo wanalitilia mashaka lazima wapige ripoti mara moja.



    Tulipanda mpaka chumbani kwa Robin ambako tuligongagonga mlango. hata hivyo kulikuwa kimya! Sammy alichukua funguo zake akaufungua huo mlango.



    Tishio tulilolipata, mwenyezi Mungu aliyetuhuruku ndiye aliyejua! Sammy alishtuka akaanguka chini. Nilipoingia mimi ndani, niliona mauaji ya kikatili ambayo sijawahi kuyaona. Robin alikuwa amelazwa kitandani huku amekufa! alikuwa amekatwakatwa na visu, kama ambavyo ingekatwa nyama. Huzuni iliniingia na uchungu wa ajabu ya kwamba nilianza kutoa machozi.



    Hatmaye Sammy alizinduka. Nilimwambia awe macho wakati nikipekua pekua kila mahali humo chumbani mwa Robin, maana huenda wakatufanya kama walivyotufanya wakati wa kifo cha John. Nilipekua kila mahali lakini sikuona lolote. Ilionekana kuwa walimuua Robin na kuchukua kila kitu walichoona kingeweza kutusaidia sisi. Chumba kizima kilikuwa kimevurugwa vibaya sana.



    Niliona kijikaratasi kidogo chini ya kitanda, nacho kilikuwa kimendikwa kwa herufi kubwa. Inaonekana hawa watu waliona hakina maana wakakitupa. Kiliandikwa "NENDA RUDI SALAMA UMEFANIKIWA, KWENDA NA MUONYESHAJI WA MAVAZI, LEO USIKU TOKA UADUINI TUNAMOFIKIRI." Nilifikiri sana lakini bado niliona haileti maana. Nilimwita Sammy aje ili naye akisome tuone kama anaweza kutoa maana yoyote kuhusu maneno hayo.



    Sammy alipokisoma naye hakuweza kuunganisha maneno hayo na kuweza kutoa maana. Kisha nilishtukia akitabasamu kwa mbali. "Hallo Willy, nadhani hiki kijikaratasi kina maana kubwa sana. Na kila jambo alilokuwa anachunguza Robin liko hapa. Huwenda Robin alijua mambo mabaya yanaweza kumtokea kwa hiyo alionelea atuachie habari kwa njia hii ya hekima hivyo kwamba bila kufikiri sana huwezi kujua ameandika nini. Willy haya maneno ya kwanza. "NENDA RUDI SALAMA UMEFANIKIWA" kama ujuavyo yana maana ya kazi yetu, maana kazi hii inafahamika kati yetu kama 'Operesheni N-R-S-U" yaani 'NENDA RUDI SALAMA UMEFANIKIWA. hivyo basi maneno haya ni kwa ajili yetu kama sikosei, maneno yaliyobaki, Robin anatueleza mambo aliyochunguza na kupata. Nadhani yana maana ya kuwa, Hizi karatasi za siri zitaenda na mmoja wa waonyeshaji mavazi wa Ureno. Yale maneno ya mwisho UADUINI TUNAMOFIKIRI yana maana ya Ureno. Kwa hiyo huyu mwonyeshaji mavazi ndiye ataenda na hizi karatasi huko Ureno leo usiku. Na kufuatana na simu uliyoipata chumbani kwa Benny, nadhani Robin yupo sawa."



    Kweli huyu Sammy ana kichwa, la sivyo ingelimchukua mtu mwenye kichwa kinene mwaka mzima kutambua inasema nini.



    Tulipiga magoti kwenye kitanda, tukamsalia Robin, Mungu amuweke mahali pema peponi. Halafu tukapaa kuendelea na kazi hii ambayo ilionekana itatumaliza. Tulifunga kile chumba, tukatelemka chini. Tulimpigia simu mkurugenzi wa upelelezi nchini Kenya kumweleza yaliyompata Robin. Alishtushwa sana na habari hizi, lakini alituambia tusife moyo tuzidi kuendelea, maana ilionekana tunaendelea vizuri sana. Alituambia kuwa atazidi kutupa msaada wowote ule tuutakao. Kisha nilipiga simu polisi kusikia kama wamepata jambo lolote juu ya Daktari Njoroge. Polisi walijibu kuwa hawakuona mwenendo wowote mbaya, ila tu ya kwamba Njoroge alitoka nyumbani kwake kama saa tatu kasorobo hivi, akaenda madukani, na akaingia katika duka moja liitwalo 'Stationary & Office Machines Ltd.' huko akanuua mashine moja ambayo inatoa 'Photostat Copies' za barua. Nilimuuliza ulikuwa muda gani umepita, akasema kama dakika kumi hivi zilizopita na kwamba alielekea nyumbani kwake 'Livingstone Green'.



    Mara moja nilipata wazo, wazo lenyewe ni kuwa daktari Njoroge ndiye 'bosi' hasa. Lakini kwa sababu yeye ni mtu mheshimiwa, juu ya ule utajiri na kisomo chake, watu hawamfikirii ubaya wowote. Baada ya kusikia utorokaji wetu usiku ameingiwa na wasiwasi sana na anaona tunaweza kumshika kabla hajaweza kupata hela zake. Kwa hiyo sasa anafikiria kufanya 'Photostat Copy' ya hizo karatasi. Na ikiwa tutaweza kuzipata hizo karatasi zenyewe, bado anaweza akapata kiasi fulani cha hela kwa kuuza zile copy.



    Tulifikiri sana tuliona jambo kubwa ni kuhakikisha kuwa hizi copy hazitatengenezwa. Na tungeweza tu kufaulu kwa kuiharibu hiyo mashine kabla ya kutengeneza hizi copy. Na pia kuhakikisha kuwa hataweza kununua nyingine. Kwa hivi tulimpigia simu mkurugenzi wa usalama ahakikishe kuwa maduka yote yanayouza mashine za namna hiyo yamefungwa mpaka kesho yake, na ulinzi ufanywe kuhusu hizo mashine. Mkurugenzi alituhakikishia kuwa hayo yatafanyika bila shaka.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mimi nilikata shauri nimfuate daktari Njoroge huko kwake kabla hajaanza hiyo kazi. Sammy ilimbidi aendelee na uchunguzi wa hawa watu ambao wamekuja kuzichukua hizi karatasi, kusudi tuweze kuzifahamu kabla ya usiku. Nilipiga simu polisi ili waniletee kijana mmoja niende naye.



    Kijana wa polisi alipokuja tuliondoka kwenda 'Livingstone Green' huyu kijana niliyepewa alionekana wa aina ninayotaka, mtulivu lakini si mchezo.



    Tulikuwa tukitumia gari la Polisi na tulipata habari wakati tukienda kwa Njoroge kwamba yeye Njoroge alifika nyumbani hapo na baada ya dakika kama tano hivi akatoka, na akaelekea pande za mjini tena. Tulipata habari hizi kwa njia ya radio ya polisi ambayo ilikuwa katika hili gari lao. Niliwambia wazidi kutueleza mwenendo wake kwa njia hii hii. Tulikwenda kulisimamisha gari letu kwenye maduka ya 'Livingstone Green'. Nilimweleza huyo kijana wa polisi abaki katika gari wakati mimi nikienda kwa Njoroge, kusudi aweze kupokea habari, na kama kutakuwa na jambo lolote kabla sijarudi akimbie kunieleza. Akanipa ramani ya mzunguko wa nyumba ya Njoroge.



    Nilikwenda bila shida mpaka kwenye hiyo nyumba. Nyumba ilikuwa kubwa na ya kibepari hasa. Kumbuka kwamba wakati huo ilikuwa ni mchana, na mambo ya mchana ni ya mchana saa hizo watu wengi walikuwa kazini nilienda na kupiga hodi. Kijana mmoja umri kama miaka saba hivi alinifungulia.



    "Kijana, mimi ni mfanyakazi wa baba yako Njoroge, ambaye huangalia mashamba yake ya Thika. Tumeonana sasa hivi njiani akienda mjini, lakini ameniambia nitakukuta wewe hapa. Na kama ulivyoona alikuja hapa na kasha lililokuwa na vitu. Ameniambia utanionyesha alipoliweka, maana humo imo mashine ambayo ni kwa ajili ya kazi ya mashamba yake huko Thika. Miye nimekuja kuichunguza kama inafaa kwa kazi yetu. Kwa hiyo nionyeshe, maana nina haraka."



    Yule mtoto bila wasiwasi alinipeleka kwenye chumba mlimokuwa na mashine nyingi na vitu vingi vya ajabu. Nilimshukuru huyo kijana kisha nikamwambia aendelee na kazi zake. Niliifungua ile mashine na kuiharibu. Kisha nikavichukua vyuma vingine ambavyo ni vya maana. Baadaye nikalifunga kasha hilo tena nikaenda zangu salama usalimini.





    Miye na Msaliti



    Tulirudi mpaka mjini tukiwa katika hilo gari la polisi. Tulipofika karibu na Pan Afrikani Hoteli, tulimwona daktari Njoroge akiwa ndiyo kwanza anarejea. Siye tuliendelea mpaka mjini. Yule kijana wa polisi alinishusha New Evenue Hoteli. Hapo nikaingia katika gari langu nililokuwa nimeliacha hapo nje ya hoteli. Nilitia moto gari langu na kuendesha mpaka Embassy hoteli.



    Nilienda nikamuona Lina, maana nilikuwa nimemwambia asitoke mle ndani ya nyumba. Nilipogonga mlango kwenye chumba sikusikia sauti. Kwa wasiwasi nilifungua mlango taratibu. Nilikutana na tishio jingine, mara hii niliona lingeweza kuniua. Lina alikuwa ameanguka chini huku ametiwa visu, kimoja tumboni, na kingine ubavuni. Sura ya hapa mahala haikupendeza hata kidogo, miye Willy. Nililia kama mama anayemlilia mtoto wake wa pekee anapokufa. Lakini kulia kwangu si kwa kawaida, maana mimi ninapodiriki kulia wewe utakuwa umezimia. silii hovyo.



    Niliuangukia mwili wa Lina. Moyo ulikuwa bado unapiga, ingawaje yeye alionekana kama amekufa. Nilivitoa vile visu, damu ikaanza kububujika vibaya sana. Nilitoa vitambaa vyangu, nikaviweka kwenye matundu ya visu. Nilimwagia Lina maji kama anaweza, kabla hajafa kabisa anieleze neno lolote na kilichotokea. Sikuweza kufanikiwa, Lina alionekana hawezi kuziduka hata kidogo.



    Nilipiga simu kwa Daktari aje mapema iwezekanavyo, ili akiweza amuokoe Lina ambaye moyo wake ulikuwa bado katika mapigo. Pia nilimpigia Sammy simu aje hapa mahala, lakini hakuweko. Niliacha ujumbe kuwa wakati wowote arejeapo aje huku chumbani kwangu.



    Nilimbusu Lina ingawaje alionekana kama maiti. Yeyote aliyefanya jambo hili lazima awe mtu aliyejua kuwa Lina ndiye aliyetutorosha toka nyumbani kwa Benny. Kama unafikiri, unaweza kujionea mwenyewe mambo yanavyonyumbulika, maana tukio hili linaonekana la ajabu sana. Hapo hapo methali moja ya kiswahili ilinijia kichwani, "umudhaniaye siye, na usiyemdhania ndiye." Sijui kama na wewe umeshaona na kukubaliana na tukio hili.



    Daktari alikuja. Alipompima Lina, alisema kwamba bado ulikuwako uhai kidogo ndani yake, lakini hayakuwako matumaini makubwa. Hata hivyo alisema atamchukua Hospitalini kwake akajaribu kumsaidia. "Huyo huenda Mungu tu ndiye ataka aishi, la sivyo ameishakuwa marehemu, maana kisu cha ubavuni kimemchoma kwenye moyo." alisema daktari.



    Nilimuomba daktari amshtue kidogo kama anaweza, kusudi huenda naweza kupata kijijambo cha kunisaidia.



    Alipomshtua Lina alitoa macho, kisha akafumba tena. Alijaribu kusema lakini akashindwa.



    "Lina ebu niambie kimetokea nini?" nilimuuliza huku nikimtingisha, maana niliona anakufa tu, kwa hiyo afadhali nipate jambo linaloweza kunifanya nimpate muuaji wake.



    "Alikuja akanitishatisha, akaniuliza...........umekwenda wapi kisha akatoa visu akanichoma........ mimi nami niliwahi kumpiga risasi lakini hakuumia sana aha........." Lina hakuweza kumaliza ila alizirai tena.



    Daktari alimchukua kumpeleka hospitalini kwake na aliniambia angejaribu kila njia kuokoa maisha ya Lina. Na kama haitawezekana itakuwa sababu ya ahadi yake. Nilitoa shilingi mia tano nikampa daktari, na nilimuaidi kumpa nyingine elfu moja akiweza kuokoa maisha ya Lina.



    Lina alikuwa amenipa pigo kubwa sana, moyo wangu ulipata kidonda ambacho Lina akifa akitapona. Nilivyomuona Lina akiondoka na daktari! Basi tu. Mungu ndiye ajuaye, maana yeye na maiti yake hakukuwepo na tofauti.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Punde si punde Sammy alitokea. Nilimweleza mambo yaliyompata Lina, naye akasikitika sana. Ilionekana sasa tumebaki siye wawili tu kufanya kazi hii. Hii ilikuwa kwa sababu ya bahati tu, maana hata siye tumekuwa tukiponea chupuchupu. Hata hapa tulipokuwa tumekaa tukizungumza na Sammy tulikuwa na wasiwasi mwingi, maana wakati wowote tungeweza nasi kuwafuata rafiki zetu John na Robin na huenda dakika hii Lina.



    "Sikiliza," alisema Sammy "Tayari nimepata habari ndogo ndogo juu ya watu wanaohusika. Binafsi ninalishuku kundi lote lililotoka Ureno kuja kwenye maonyesho. Kwanza, wale wanawake wa Ureno waliokuwa wakionyesha mavazi walionekana kama kwamba si kazi yao ya kawaida. Pili, wamekuja vijana watatu pamoja na hao wanawake. Vijana hao tangu waje hawajaonekana hata kidogo ila tu wameweza kuonekana hotelini kwao. Tatu, Robin alikuwa amepata habari kamili kuwa wao ndio ambao wamekuja kuchukua hizi karatasi kabla ya mauaji yake. Nne, kijana mmoja wa polisi ambaye tulimweka kumvia Benny, amesema kuwa Benny alienda mchana huo kama mara mbili hivi kukutana na hao waonyeshaji mavazi toka Ureno.



    Hizi sababu za Sammy zipo katika usawa wa mia kwa mia. Kwa hivyo sasa lililopo ni kuhakikisha kuwa kwa njia nzuri ama mbaya siye ndiyo tunazichukua hizo karatasi badala yao.



    "Je, yule kijana wa polisi aliyekuwa akimfuata Benny leo hii mchana, alisema lolote juu ya Benny kuja hapa Hotelini kwangu?" nilimuuliza Sammy.



    "La, alisema Benny hakusogelea sehemu hizi maana alionekana mwenye shughuli nyingi sana.



    Jibu hili lilinipa uhakika wa jambo fulani ambalo nitakapokwambia utastaajabu. Lililokuwepo sasa ni kuwatafuta Benny, Lulu na 'Bosi' kabla hawajafanya upuuzi mwingine wowowte, maana tusipowawahi sisi, wao watatuwahi.



    Kabla hatujafanya jambo lingine lolote ilinibidi niandike ripoti kwa Chifu nikimweleza habari ya mambo yote yalivyo mpaka sasa. Maana sasa tumefikia karibu hatua ya mwisho na hii hatua ndiyo mbaya zaidi, maana kila kundi linapigania kushinda. Na hii ina maana ya vifo vingi sana. Nilimweleza Chifu mambo yote tangu mwanzo mpaka ambapo tumefikia, kisha nikaifunga na kuitia kwenye kisanduku changu cha barua za kutumwa.



    Kisha nilivalia ili tuondoke. Tulijitayarisha kufa na kupona. Wote tulivalia furana ambazo risasi haziwezi kupita,'bullet proof' kisha tukavalia juu kama kawaida. Hizi furana tulikuwa tumezipokea mchana huu toka kwa Chifu baada ya kumwomba wakati tunaona hatari zinazidi. Tulipokuwa tunataka kutoka simu ililia.



    "Hallo, huyu ni Peter, wasemaje Willy."



    "Miye salama tu mheshimiwa, je una utenzi?"



    "Ndiyo nina jambo la kukueleza, na ni la siri zaidi. Ni jambo la kuweza kukusaidia sana."



    "Niambie basi Peter mpenzi."



    "Hapana, kwenye simu mambo huwa si mazuri sana, kwa hiyo tafadhali njoo hapa."



    "Vema nakuja sasa hivi kama muda wa dakika kumi hivi." Tulionelea tusiende wote kwa Peter ila Sammy aende kutalii kama Lulu yupo hapo Hotelini kwake. Na huko akamtishe ili aweze kutoa habari zozote. Kisha baada ya hapo Sammy angekuja hotelini kwa Peter, na hapo ndipo mahala ambapo tungekata jinsi ya kuendelea. Tuliagana tukatakiana bahati njema.



    Nilienda zangu mpaka 'New Stanley Hoteli.' Nilipokuwa nikipita hapo chini, niliona jamaa wengi wakijiburudisha katika 'Thorn Tree. Lakini pia nilimuona kijana mmoja miongoni mwa hao watu ambaye aliponiona aliinama kidogo ili nisiweze kumfahamu. Lakini ilivyo macho yangu ni hatari, maana katika nusu nukta, nilikuwa nimeishaona kila mtu mwenye umati wa watu elfu moja. Huyu kijana nilimuona kule hotelini 'Intercontinental' wakati wamekuja na Benny huku wameshikilia bastora. Nilijifanya na mimi sikumuona nikaendelea zangu kumuona mheshimiwa Peter.



    Nilipofika kwenye chumba cha Peter niligonga akanikaribisha ndani, "karibu Willy, asante sana kwa kufika!!" alisema akaenda kwenye kabati kuchukua vinywaji.



    "Asante sana kwa kunikaribisha Peter, lakini miye sitaki vinywaji vyako maana nina kazi nyingi sana," alikuwa bado akimimina pombe akidhani huenda natania kusema kuwa sitaki, "kwanza lazima nihakikishe kuwa nimewatia nguvuni waalifu wote na wengine kuwaua. Wewe ukiwa wa kwanza wa hao waalifu!" Peter ghafla aliangusha chini chupa ya pombe akageuka kunitazama. Alipogeuka alikuta tayari nimeshatoa bastola mbili kumwangalia. Huenda nikadhaniwa mimi ni mkichaa, lakini la, kila siku nikisema neno au nikishuku neno jua niko sawa.



    "Unamaanisha nini Willy, wewe unajua vema kuwa mimi ni mpigania uhuru halisi, na hasa nimepewa cheo kwa ajili ya uhaminifu wangu!" alisema huku akitetemeka kwa hofu.



    "Ulidhani wewe ni mjanja sana Peter, yakwamba ungeweza kuuza wenzako bila kutambuliwa. Na kweli kidogo ungefaulu katika mambo yako, kama usingefanya makosa fulani fulani, na pia kwa sababu walimweka Willy katika kazi hii ambaye anashuku kila mtu. Hata pia nakusifu kwa akili zako nyingi, lakini nasikitika kwa kushindwa kwako."



    "Ulijuaje ya kuwa mimi nilikuwepo kwenye mpango huu?"



    "Tangu siku ya kwanza niliyoondoka Dar es Salaam nilijua lazima kuwe na mtu ambaye kwanza ana cheo kikubwa sana kwenye Ofisi ya wapigania uhuru ambaye anashiriki katika tukio hilo.



    "Kabla sijatoka Dar es Salaam nilienda nikakagua ile ofisi yenu iliyobomolewa, na ilionekana kuwa mle ndani vitu vingine vyote havikuguswa ila kabati lile lenye karatasi tu. Hii ilionyesha waziwazi kuwa lazima hawa watu wamepata habari kamili ya mahala karatasi hizo zilimo laasivyo tungekuta vitu vyote humo ndani vimevurugwa vurugwa kutafuta mahali zilipo hizo karatasi. Pia ilinipa wazo kuwa lazima awe afisa mwenye cheo kikubwa sana kujua hata mahala karatasi za siri kama hizo zilipotunzwa, maana afisa wa vivi hivi tu asingeweza kujua.



    "Na kama unakumbuka siku ile usiku nilipokuwa nikienda kwa Chifu ulikuwa ukinifuata. Ulijifunga shuka na huku umevaa miwani myeusi. Gari lako halikuwa na nambari. Nilijua tu kuwa huyu mtu lazima ananifahamu ndiyo sababu anajibadili hivi.



    "Wewe mwenyewe ulikuwa umekuja na hili kundi la akina Benny. Na baada ya kufanikiwa kuziiba hizo karatasi wao waliondoka wewe ukabaki Dar es Salaam. Ulibaki kwa sababu ulikuwa na wasiwasi ya kwamba wangeweza kuniweka mimi kwenye kazi hii. Hivyo ulivizia uone na ulikuwa sawa.



    "Kisha ulinifuata Nairobi baada ya mimi tu kufika. Maana nilikuwa nimeweka mtu wa kuchunguza mpigania uhuru yeyote mwenye cheo ambaye angeingia Nairobi siku ile. Na wewe ulionekana ukitoka Dar es Salaam." Wakati huo huo wote bado nilikuwa nimeshikilia bastora zangu tayari tayari, na Peter alionyesha mshangao wa ajabu machoni mwake.



    "Ulipofika hapa." Niliendelea, "Ulimuona John na kwa sababu mlikuwa mkifahamiana. John alikwambia kuwa alikuwa amekuja kwa tukio hilo. Hakusita kukueleza sababu kwamba anajua wewe ni afisa mkubwa sana katika ofisi ya wapigania uhuru. Uliripoti mambo hayo yote kwa Benny na Njoroge, na wao wakakuamuru umuue John. Ulifanya mpango ukamuua John."



    "Umejuaje kuwa Daktari Njoroge ndiye 'bosi'" aliuliza.



    "Hiyo ni rahisi. ngoja niendelee kukueleza jinsi ambavyo wahalifu hawana akili, hali wakifikiri wana akili sana. Kisha ukamweleza Benny na Njoroge juu yangu - kuwa mimi pia ni hatari zaidi. Kwa hiyo jambo la kufanya ilikuwa wewe ukimbie upesi upesi kujifanya kuwa unatusaidia wakati unatuwinda.



    "Nilipohakikisha ya kwamba ni wewe msaliti, hata mimi nilianza kukufanyia ujanja. Siku nilipotoka na Lina pale 'City hall' ni wewe tu uliyejua. Ulienda ukamwambia Benny, Benny akaweka mtu wa kutuvizia. Bahati mbaya miye nilitambua nikamkomesha.



    "Wakati ninaenda kwa Lulu jana usiku nilikukuta 'Hotelini Intercontinental' na wageni fulani fulani, na ni wewe tu ulijua miye nimeenda humo. Ukaenda ukampigia Benny simu kuwa niko huko, akanifuata. Lakini mimi nilikuwa nimejua kitambo kuwa wewe utafanya jambo kama hili kwa hivi nikamwahi.



    Halafu tulipotoroka kule kwa Benny baada ya kutushika. Benny alikupigia simu akikueleza kuwa tumetoroka lakini hakujua ni nani aliyetusaidia kutoroka, kwa hivi akakwambia unipigie simu kijanja niweze kukueleza. Nami nikiwa na nia ya kuzidi kukupumbaza zaidi nilikueleza habari zote.



    "Ulipomweleza Benny juu ya Lina akakuambia umtafute mpaka umempata uweze kumuua. Yeye hakutaka kufanya jambo kama hili maana kwanza alijua waziwazi kuwa Lina si mchezo, huwezi kumuendea hovyo hovyo. Pili alifikiri Lina anaweza kuwa yupo chumbani kwangu na kama kwa bahati mbaya angetukuta wote chumbani angejua maafa ambayo yangewapata.



    "Wewe ilikuwa ni rahisi kuja kwangu, maana kama kwa bahati ungenikuta nipo ungejifanya kuwa unakuja kwenye mazungumzo tu. Bahati nzuri hukunikuta. Ulipofika chumbani kwangu ulimkuta Lina, na kwa vile Lina hakuwa anakufahamu mara moja alikuja juu, lakini ulimuwahi ukamtia visu." Wakati huu alionekana kustaajabu sana juu ya habari hii.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Lina naye aliwahi kukufyatulia risasi mkononi. Kuona hivyo ukakimbia kabla ya kuhakikisha sawasawa kama Lina amekufa ama vipi." nilimwendea nikamvua shati lake, nikakuta kweli wamemfungafunga kwa vitambaa. Kisha nilijiegemeza kwenye ukuta huku nimeshikilia bastola zangu kama kawaida. "Halafu uliponipigia simu nije nikuone ndicho kilikuwa kifo changu na mimi, maana kuna watu ambao unajua watakuja humu wakati wowote. Wewe hukujua kama mimi najua, hivyo uliwaambia wakae kwa muda kidogo ili uweze kunipa pombe, na nisifikirie habari yoyote kusudi iwe rahisi kwenu kupambana nami. Lakini hapo ndipo ulipopiga chini hasa, maana Willy, alikuwa anajua kila kitu. Kwa hiyo nimekuja kwenye kifo chako si changu. Na nadhani taarifa nitakayoitoa kwa mkurugenzi wa wapigania uhuru itamfanya atoe machozi. Kwani kweli siye waafrika tunakulana kama samaki. Wahenga walisema kikulacho kimo nguoni mwako." Na ni kweli kabisa."



    "Mh, kumbe unajidanganya sana Willy unadhani utatoka humu salama? wala usidhani kwamba wahalifu wanapofanya jambo kubwa kama hili huwa wanalifanya kwa pupa. Kwanza wanaambiana njia zote ambazo wanaweza kupita, na jinsi ya kuzuia pasiwepo na uwezekano wowote wa kuingiliwa." Alisema Peter huku sasa amekaa kitini."



    "Wewe walikuahidi kukulipa kiasi gani Peter."



    "Lazima waliniaidi fedha nyingi laasivyo nisingelikubali kuhalibu jina langu na kuuza watu wangu."



    "Lakini kiasi gani hebu nipe jumla laasivyo naweza kugeuka mbogo sasa hivi, nikakutia marisasi maana unanijua waziwazi nilivyo."



    "Wangenilipan shilingi milioni kumi."



    "Na malipo yote ya hizo karatasi ni kiasi gani?"



    "Ni shilingi milioni mia moja."



    'Zimeishafika hapa toka Ureno?"



    "Sijui kama zimefika," alijibu huku akiwa na wasiwasi. niliachia risasi moja na kukipiga kiganja chake.



    "Sema kweli, maana wewe, Benny na Daktari Njoroge ndiyo mnaojua ukamili wa habari hii."



    "Ndiyo imeishafika, ilifika jana usiku, lakini bado walioileta hawajatupa, watatupa leo usiku."



    "Watawapea wapi?"



    "Kusema kweli hapo sijui," alijibu kwa hofu tena. Nilimtia risasi nyingine ya mkono karibu na pale Lina alipokuwa amempiga. "Wapi, niambie laasivyo utakufa."



    "Sijui kwa kweli, lakini nadhani itakuwa wakati wa maonyesho huko 'City hall'."



    "Hizo karatasi zimewekwa wapi?"



    "Kule kwa .........." kabla hajamaliza usemi vijana wawili waliingia kupitia dirishani. Nilipogeuka kuwatazama, wengine wanne waliingia mlangoni. Peter alisimama na kukimbia kabatini alikotoa bastola na kuishikilia. Kisha wakaja vijana wengine wanne, wakawa kumi. wawili wengine wakaja lakini wakabaki mlangoni mimi nilikuwa bado nimebaki nimesimama hivyo hivyo na huku bado nimeshikilia bastora zangu wote walikuwa wamejipanga upande mwingine wa ukuta wote wakiwa wameshikilia bastora zao.



    "Tupa chini hizo bastola zako Willy, maana naona kifo chako kimefika," alisema Peter kwa sauti ya ujuvi. "Vipi, huwezi ukajihudhunikia mwenyewe, kabla mimi sijafa wewe mwenyewe utakuwa tayari umeishakufa. Ha ha ha ha, mbona nyie wapelelezi hamkubali kushindwa! watu kumi na watatu na wewe mmoja bado unapanua domo lako. Kuzungumza upuuzi mtupu. Wewe utakufa, miye nitapata fedha na hakuna atakayetambua kuwa miye Peter nilihusika na mambo haya."



    "Unajidanganya sana. ukiniua mimi lazima Sammy atakupata tu."



    "Ohooo! Umechelewa sana rafiki yangu, sammy ameishakamatwa huko chumbani kwa Lulu. Benny amemchukua huenda sasa ameishakuwa majivu," alijibu mmojawapo wa wale watu.



    Niliona kuwa huyu kijana hakuwa anatania. Nilikata shauri mara moja nipambane nao. Ikiwa nitakufa basi, lakini ikiwa nitapona nitahakikisha kuwa nimemponyesha Sammy nikimkuta bado hai.



    "Fyatueni bastola zenu sasa mbona mnaogopa? mnaonekana mkitetemeka. Mkichelewa basi nitawamaliza miye kabla hamjanimaliza. Yaonyesha kwamba mnao uwoga wa kike," nilisema hivi kusudi niwatie hasira, maana mtu akipatwa na hasira hawezi kuona sawasawa. Maneno yangu yalifanikiwa maana niliona wanapandwa na hasira hovyo hovyo.



    Peter alitoa ishara huku akisema, "Kwa heri Willy, nitahakikisha kuwa nimerithi mali yako yote hata Bella. Fika salama huko ahera."



    Walipotaka kuanza kunifyatulia risasi haraka nikawafyatulia mfululizo. Sita tayari chini. Niliipiga risasi mikono ya Peter akaanguka chini bila ya kuwa nayo bastora. Kisha nikawamaliza wale wanne waliobaki. Nilimsikia Peter akitoa sauti ya kuwaita wale wawili wa mlangoni. Walipokuja wakanikuta miye tayari nawangojea. Nikawafyatulia kisha nikawavutia ndani na kufunga mlango kisha nikamfuata Peter.



    "Eh, umejua kuwa mimi ni Willy, eh Peter? uhalifu haulipi. Na mshahara wa dhambi wa mauti bali karama ya Mungu ni uzima wa milele."



    "Oh Willy nisamehe, nilivutiwa na pesa. Oh nimetubu nimetubu."



    "Pesa, pesa Peter! unakubali kuuza Afrika nzima kwa ajili ya pesa, ona sasa umepata nini ndani yake!



    Peter alianza kulia.



    "Zile karatasi ziko wapi?"



    "Kule kwa Daktari Njoroge katika stoo yake. Zimewekwa katika sefu ya chuma humo stoo. Na watazibadilisha leo saa mbili na dakika kumi, lakini sielewi wapi."



    "Sasa Peter, kwa heri ya kuonana. Nitakupa risasi sita kwa sababu ndivyo nilivyoaidi nilipokuta John ameuawa. Nitakutia visu viwili kama kisasi kwa ajili ya msichana Lina kama nisingelikuwa nimeapa ningekurudisha Dar es Salaam wakakuweke kitanzi. Kwa heri kwa mara ya pili."



    "Ohoo nisamehe Willy..........."



    Niliondoka mpaka kwenye mlango kisha nilimuendea na kumtia visu viwili hatimaye nikaachia risasi sita kama yeye alivyoziachia kwa John na kama alivyo mchoma Lina.



    Lo. furana yangu "buletproof" ilikuwa imeniokoa vizuri sana.



    Niliondoka mle ndani haraka mpaka chini. Mawazo yangu sasa yalikuwa kwa Sammy, kwamba nitamkuta mzima ama vipi. Wameelekea upande gani sijui. Niliona nianzie kule kwa Lulu alikokwenda. Nilienda na gari langu mpaka hoteni kwa Lulu. Nilipanda mpaka kule chumbani kwa Lulu. MLango ulikuwa umefungwa. Nilipoingia ndani niliona kazi ya Sammy. Niliona Maiti nne zote zimekula visu.



    Nilikaa kwenye kitanda nikifikiri wapi wamempeleka lakini sikuwa na mwangaza wowote. Nilizunguka huko na huko chumbani. Hofu, wasiwasi, uchungu, fikira, huzuni, vyote hivyo viliusukasuka moyo wangu, chuki na maudhi niliyokuwa nayo yangeweza kunifanya nizimie. Niliona karatasi kwenye kitanda. Nilipoiendea mwandiko haukuwa wa Sammy ila mtu mwingine. UPESI, NAIROBI SOUTH, WILISON AIRPORT, KABLA YA SAA MBILI KWENYE NYUMBA MOJA NAMBARI B 141. RANGI BLUE TAFADHALI UFANYE HARAKA LAA SIVYO UTAJUTA KUCHELEWA KWAKO."





    'Lililo na mwanzo lina mwisho "Bosi"



    Niliwaza harakaharaka kama huu ni mtego ama vipi. Lakini hata kama ni mtego niliona huenda unaweza kunisaidia. Sammy hakuwemo humo chumbani hivyo nikawaza kwamba pengine wanaye huko waliko au ameisha uawa na kutupwa mahala pengine. Zaidi niliona lazima wameenda naye huko waliko. Basi mwishowe nilikata shauri nifanye kama vile ilivyoelekezwa katika kile kikaratasi. Ilikuwa yapata saa moja kasorobo sasa.



    Nilionelea katika hizo dakika kumi na tano nikimbie kule hotelini kwangu, nikaoge upesi upesi kisha nibadilishe mavazi maana shati langu lilikuwa limetobolewa tobolewa kwa risasi. Nilienda nikakoga haraka haraka, nikabadilisha shati na kuondoka zangu kuelekea Nairobi South.



    Nilifika "Wilson Airporot" kama saa moja hivi. Kulikuwa na ndege moja tu hapo kiwanjani. Nilisimamisha gari langu, halafu nikatoka na kuanza kutafuta ile nyumba ilikokuwa. Mahala pote palikuwa kimya, baridi ilikuwa kali sana, na moyo ulikuwa unanipiga mno. Nilitafuta kwa muda mrefu kisha ndipo nikaiona. Wakati huo palikuwa pameisha kuwa giza mahala pote.



    Moyo wangu ulizidi kupiga na nilinuia usiku huu huu ikiwa nikiwa mzima lazima nihakikishe 'Operesheni N-R-S-U' imefanikiwa. Niliiendea ile nyumba pole pole huku nikichunguza huku na huko. Mawazo yangu yote yalikuwa juu ya Sammy kama ni mzima ama ameuawa.



    Nilikuwa nimeisha kata shauri kuua kitu chochote kitakachokuja njiani pangu kabla sijaweza kufahamu nini kimempata Sammy.



    Nilijua kama ile karatasi ilikuwa mtego basi watakuwa wananingoja lakini kama hapana basi watakuwa wanadhani kuwa miye nitaenda kumtafuta Sammy kwa Daktari Njoroge huko 'Lavington Green', au kwa Benny huko "Westlands'. Nilipozungukazunguka nikakosa kumuona mtu yoyote hivyo nikadhani huenda hawakuwa wakinitegemea. Nilijibanza kwenye ukuta, halafu nikachungulia kwenye dirisha moja; taa zilikuwa zikiwaa humo ndani ya chumba. Nilipochungulia zaidi humo ndani nilimuona Sammy amelazwa kwenye kitanda na amefungwa kwa kamba. Pia alionekana akiwa bado amezimia. Moyo wangu ulifurahi sana na ukanipa nguvu zaidi kuona Sammy alikuwa bado anaishi, ingawaje chini ya hali ya mateso ya ajabu.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Niliwaza jinsi ya kuweza kuingia humo ndani lakini nilishindwa. Dirisha lilikuwa na vyuma ambavyo nisingeweza kuvifanyia jambo lolote! mwishowe nilijitolea nipitie mlango wa mbele, nilikuwa tayari na bastora zangu. Kijana mmoj alikuja kufungua mlango. Nilimpiga ngumi ya shingoni akazirahi papo hapo hata hakuweza kutoa sauti.



    Niliingia ndani nikafika kwenye mlango wa sebuleni. Huu mlango ulikuwa wa mbao lakini juu ulikuwa na kioo, Nilipoangalia ndani nikawaona Benny, Lulu na watu wengine kama kumi hivi wote wakinywa kwa furaha sana. Nilifikiria niingie lakini sikuona jambo la maana, maana 'bosi' hakuwemo na bosi ndiye mwenye vitu ninavyovitaka. Hawa watu humu ndani walionekana wameridhika sana na mambo, ila Lulu mara kwa mara alikuwa akiangaza macho huku na huko.



    Kisha wazo likanijia, nikarudi nje taratibu ili nikawe tena kwenye lile dirisha la chumba alimo kuwa amefungiwa Sammy. Kabla sijaenda, nilimbeba yule mlinzi wa mlangoni nikamsukumia kwenye mfereji wa maji halafu nikahakikisha kuwa haamuki mpaka baada ya siku tatu hivi.



    Nilipofika pale dirishani, nilikata unyasi mmoja mrefu sana hivi ambao nilijua utamfikia Sammy hapo alipolala kitandani. Kweli ulifika. Niliusukumasukuma sikioni mwake mpaka akazinduka. Alipozinduka alitazama akaniona. Alitaka kusema jambo nikamfanyia ishara anyamaze, maana alionekana akili zake bado hazikuwa zinaweza kuunganisha mambo. Kwa sababu mimi ni namwelewa Sana Sammy, nilijua haitamchukua dakika nyingi kabla ajaweza kuelewa nini ni nini.



    Baada ya muda kidogo niliona anaanza kutambua mambo, alinitazama akanitingishia kichwa kuonyesha kuwa sasa anaanza kuelewa mambo. Ilionekana kama akina Benny walikuwa wamemponda vibaya sana Sammy hata kuzirai muda wote ule. Na pia ilionekana akina Benny walijua itamchukua muda mrefu sana Sammy kuzinduka ndiyo sababu hawakuwa na wasiwasi.



    Nilishawambieni kuwa Sammy ni maarufu kwa visu. Kwa hiyo alinifanyia ishara nimtupie visu ili aweze kukata zile kamba na kujifungua. Ungeweza kustaajabu angezikataje zile kamba maana hapo mwanzoni nilikuwa nimekwambia kuwa walikuwa wamemfunga vizuri sana. Lakini usitie shaka nitakuelelza sasa hivi.



    Kichwa cha Sammy hakikuwa kimefungwa yaani kuanzia shingoni. Basi nilimtupia kisu toka dirishani nacho kikaanguka karibu sana na mahali alipokuwa. akajikurupusha huku na huko hadi akafanikiwa kukiuma kwa midomo. Sammy akakata zile kamba kwa kutumia mdomo. Kile kisu ni kikali sana fahamu, hata niseme zaidi ya wembe. Kisha nilimtupia visu vingine kama sita hivi nilivyokuwa navyo. Tulifanyiana ishara ambazo ni sisi wenyewe tu tunazozifahamu.



    Miye nilirudi mpaka kwenye mlango wa mbele nione kama ninaweza kufanya lolote. Ilivyokuwa inaonekana mpaka sasa, ni kuwa mahala pa kukutania kati ya Benny, Bosi na wale waliotumwa kuja kuzichukua hizi karatasi ni hapo. Na pia ilivyoonekana hawa watu wataondoka na ndege ndogo kuelekea kwao, ndiyo sababu wakachagua nyumba ya kukutania karibu na kiwanja hiki.



    Bado nafikiria la kufanya nikasikia sauti nyuma yangu, na nikasikia mdomo wa bastola unanigusa, "Haya tembea mheshimiwa, kama unadhani kuviziavizia nyumba za watu kunasaidia."



    Sikuwa na la kufanya ilinibidi nifanye kama nilivyo ambiwa. Mlango ule unaoendea sebuleni ulikuwa umefunguliwa nikaingizwa ndani.



    "Karibu Willy, nafurahi sana kukuona tena baada ya kunitoroka jana kwa namna ya ajabu. Nimefurahi kuwa nyie watu hamnipi shida ya kuwatafuta ila mnajileta wenyewe. Kaa chini hapo tuweze kuzungumza kidogo kabla ujashuhudia kwa macho yako jinsi tutakavyofulu." alisema Benny kwa maringo na taratibu sana.



    "Asante sana kwa kunikaribisha Benny, lakini nasikitika sana kuwa hutafaulu katika mipango yako, aidha sitakaa nishuhudie ukifanya unyama mimi nikitazama tu." nilimjibu kwa utaratibu mwingi pia.



    Nilikuwa nikiwapa maelezo mengi hayo kusudi waweze kumsahau Sammy kwa muda na hii ingempatia muda wa kuweza kujifungua na kujinyooshanyoosha aweze kuwa tayari kwa vitendo.



    Ilipofika kama saa mbili kasoro dakika ishirini hivi. Daktari Njoroge akiwa na walinzi kama wanne hivi aliingia.



    Huyu Daktari Njoroge ni mtu mwenye umri wa makamo kama miaka arobaini na mitano hivi. Jinsi mwili wake ulivyokaa unaonyesha utajiri mtupu. Nilipata habari kuwa amesoma sana, na amehitimu kama Daktari huko Uingereza. Uso wake uonyesha furaha kila wakati. Pia uonekana kuwa anatoka katika ukoo ulioendelea vizuri sana.



    "Karibu 'bosi' nadhani utafurahi sana nikikutambulisha kwa kiumbe ambaye kwa wakati wote huu amekuwa akitutia wasiwasi sana, lakini sasa tena amejileta na yuko chini ya mikono yetu," alisema Benny kwa furaha kubwa.



    "Endelea Benny, tuweze kufahamiana kabla hajazikwa," alijibu 'bosi'



    "Huyu ni mpelelezi maarufu katika Afrika nzima, bwana Willy Gamba, ambaye anafanya kazi na Idara ya Uchunguzi ya Tanzania, lakini mara nyingi; anafanya kazi bega kwa bega na Idara za aina hii hii za hapa Afrika ya Mashariki."



    "Aisii, mimi naitwa Dr. Dickison Njoroge, tajiri sana katika Afrika Mashariki nzima. Na nimekuwa tajiri hivi kwa ajili ya shughuli za namna hii bwana Willy, kwa hiyo kuniingilia kwako kulikuwa kunapoteza muda na fedha yangu. Lakini hata hivyo napenda sana mioyo yenu ilivyo migumu ya kwamba hata naona wivu. Ubaya ni kwamba, ushujaa wako mwisho wake ni hapa. Na kabla sijaona unakufa, nataka kukuonyesha jinsi miye nilivyo na akili nyingi, na jinsi kundi langu lilivyoundwa kwa uimara kabisa." alisema Dr. Dickison Njoroge hali akinitazama kwa furaha.



    "Siye tuna chama chetu, nacho ni kikubwa sana, kinao wanachama katika Afrika Mashariki nzima. Pia kina uhusiano na vyama vya namna hii hii katika Afrika na hata nchi nyingine za Ulaya. Hapa Afrika ya Magharibi, mimi ndiye rais wa chama hiki na kesho nategemea kuita mkutano ambao nataka tumchague Benny kama Katibu Mtendaji wa chama badala ya Job ambaye mlimuua katika msukosuko huu. Na pia nataka nikueleze waziwazi kuwa chama hiki kina wanachama pia kutoka hata Serikalini. Watu wenye vyeo vya juu kabisa wana hisa katika chama hiki. Kwa hivi ndiyo sababu kila siku siye hatuwezi kushindwa maana "Zimwi likujualo halikuli likakwisha" walisema waswahili.



    Katika wizi wa karatasi hizi, mtindo wetu ni ule ule umetumika. Maafisa wetu wa Tanzania na Uganda wote tulishirikiana bega kwa bega mpaka tukafaulu. Na leo baada ya saa mbili na dakika kumi, chama chetu kitakuwa tajiri kuzidi vyama vingine vyote. Siye tunafanya kazi sawa sawa na jinsi nyie kwenye idara ya upelelezi mnavyofanya. Na pia tuna watu mashuhuri kama wewe na wengine kutoka katika idara yenu.



    "Miye najua mpaka sasa mnajua tulivyozipata hizi karatasi, lakini najua hamjui jinsi ambavyo zitapelekwa na wapi zitapelekwa."



    "Tunajua Daktari Njoroge usijivunge kuwa akina siye hatujui, hata ambavyo unajidanganya utafanya usiku huu pia tunajua," nilimjibu huku sauti yangu ikionyesha dharau kubwa.



    "Kama unajua basi sijali hata chembe, maana wewe sasa ni sawa na maiti, na kama maiti inajua jambo nani huyo atakayejali?



    "Ulipokuja kwangu na kuharibu mashine yangu, nilipopata habari nilichukia kiasi kikubwa sana ya kwamba miye mwenyewe nataka kushuhudia kifo chako, na pia kwa sababu wewe ndiye mtu wa kwanza kuweza kunigundua mimi nikiwa kama kiongozi wa kundi la wahalifu. Kwa kifupi Bwana Gamba ni kwamba, muda wa dakika ishirini hivi siye tutakuwa watu tajiri kabisa.



    "Hizi karatasi zinanunuliwa na watu wa Ureno kwa kiasi cha shilingi milioni mia moja na siye tumezipata kwa kuuza maisha ya watu wetu wengi. Na Serikali imezitafuta kwa gharama iliyo kubwa kiasi cha kutisha. Kadhalika imepoteza watu wake mashuhuri kwa ajili ya hizi karatasi na bado wasizipate.



    "Mnamo saa mbili kamili, wapelelezi fulani toka Ureno tunaonana nao hapa hapa ndani, na naona zimebaki dakika kumi kufika muda huo, na wakati huo nitahakikisha kuwa nyie mtakuwa mmeishakufa. Hao vijana wakitupatia fedha na siye tutawapatia hizi karatasi. Nao wataondoka na ndege yao moja ambayo itawachukua hapa hapa kiwanjani wakiwa kama watu waliokuja katika maonyesho ya mavazi na ambao kwa sasa wanamaliza maonyesho yao na wanarudi nyumbani. Kwa hivyo hakuna binadamu yeyote ambaye atawatilia tuhuma.



    "Wakati wakifika Ureno miye na wenzangu tutakuwa tumegawana fedha, tunakula raha tu. Halafu wapigania uhuru watakapoanza kupigwa naweza kutoa kiasi cha shilingi milioni moja kuwasaidia. Na nakwambia nitatangazwa dunia nzima kama mtu mwenye moyo wa pekee na mwafrika safi. Siku moja utakapofufuka ukiwaambia kwamba mimi ndiye niliyewasaliti kwa kuziiba hizi karatasi na kuwapa wareno nao wakapigwa vibaya sana, watakushitaki kwa kusema uongo maana tayari watakuwa wananiabudu kama MUNGU wao mdogo kwa kuwasaidia kiasi hicho. Unaonaje si hekima nzuri sana hiyo?"



    "Kwa kweli ni hekima nzuri kama ungefanikiwa, Lakini kwa Sababu hutafanikiwa, hata mimi nakuonea huruma ya ajabu. Ni afadhali usingezaliwa bwana Njoroge maana yatakayokukuta hata watoto wako watajichukia kwa nini walizaliwa na baba kama wewe," nilijibu kwa kiburi sana ingawa sikuwa na bastola hata moja. Bastola zangu walikuwa wameishaninyang'anya.



    Nilikuwa na uhakika kuwa, wakati huu lazima Sammy ameishakuwa tayari, alikuwa tu anangoja kuwagutusha. Lulu alikuwa akinitazama kwa macho ambayo yalikuwa yananiambia hadithi za sungura nilizozisoma darasa la tatu. Alikuwa naye ameshikilia bastola mikononi mwake. Benny na vijana wengine walikuwa na furaha ya ajabu maana 'bosi' alikuwa akiwatukuza namna ya jabu.



    Kamfungulieni huyo mbwa mwingine humo ndani, nadhani atakuwa bado amezimia, nataka kuwaona wanakula marisasi mbele yangu mwenyewe. Maana naona huyu Gamba ni mshenzi kiasi cha kwamba hanitambui sawa sawa. Kuwa rais wa chama kama hiki, lazima atambue kuwa mimi ni mtu wa pekee, na pia mwenye busara za pekee," alisema 'bosi' huku akimtazama Benny.



    Benny alimueleza kijana fulani hapo akafungue mlango - Lulu tu ndiye alionekana hana furaha, huku rangi yake ikizidi kubadilika. Nilidhani huenda anachukia kuona bado naishi. Nilimtazama huku nikitabasamu kisha nikamwambia, "Wewe malaya unachelewa kwenye maonyesho, watu wanakungoja ukawaonyeshe mwili wako huo usio na bei. Mana ni mtu fisadi tu ambaye hathamini mwili wake kiasi cha kuonyesha kwa kila mtu." Lulu hakujibu neno ila tu alitazama chini.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Benny aliniangalia kwa hasira nyingi akasema, "wewe rafiki yangu, huwezi kumwadhiri mke wangu kiasi hicho hali mimi nipo hapa. Hiyo dharau kubwa sana mshenzi wewe."



    "Yeeeeeeya, wewe kweli uko nyuma, unadhani huyu fisadi anaweza kukaa na wewe! humjui nini, mbona hukuniuliza zamani nikueleze, maana mimi nina historia yake toka A mpaka Z." nilisema huku nikicheka sana.



    Benny alitaka kusema neno lakini kabla hajasema, yule kijana aliyeenda kufungua mlango wa chumba ambamo alifungiwa Sammy alianguka chini na kisu kifuani. Wote walisimama na kuanza kutoa risasi upande ule wa chumba miye niliruka nikaanguka chini ya sofa.



    Mle ndani mlikuwa na watu kama kumi na watano hivi wa upande wao. Na miye nilijua Sammy ana visu sita kwa hiyo nilijua watu sita watakuwa wameishakufa kabla hawajatuandama. Lulu alisimama kama anataka kukimbia halafu kwa bahati mbaya akaangusha bastola yake kwenye kichwa changu. Basi niliona sasa tumeishaokoka, maana kama Sammy ataua sita miye wale wengine nitawafanya kazi kabla hizi risasi hazijaisha. Risasi sasa zilikuwa zinapigwa upande wangu na kule mlangoni kwa Sammy. Sammy alifanya mlango kama ngao yake.



    Mimi nilianza kazi. Niliposimama niliona watu watano wameishaanguka. Basi miye niliwalisha waliokuwa karibu yangu. Nilipoona mwingine anakula visu nilijua sasa Sammy ameishiwa visu kwa hiyo ilikuwa sasa ni kazi yangu kumuokoa Sammy. Nilijaribu kumpata Benny lakini wapi. Wengi wao walikula risasi mpaka nikaona wamebaki wanne. Benny, Lulu, 'Bosi' na kijana mwingine. Walipoona mambo yamewazidia, walionelea wakimbie. Kweli walikimbia na kupotelea gizani.



    Nilimfuata Sammy, nikampa heko kwa kazi yake nzuri aliyokuwa ameifanya kwa wakati huo. Aliniuliza nilipataje bastola nikamweleza iliangushwa na Lulu kwenye kichwa changu wakati nikijificha nyuma ya sofa kuzuia risasi.



    "Miye sikubali kuwa aliiangusha kwa bahati mbaya Willy, kila siku nakwambia wanawake wazuri ni sumu huenda ana jambo, maana tangu wanishike kule kwake tabia yake Lulu imenishinda. Jinsi anavyojiheshimu ni ajabu."



    "Hata mimi nimemuona hakuwa na furaha wakati wengine wote walipokuwa wanafurahia sana. Sasa tufanye nini Sammy, maana hatujui hawa watu wamekimbilia wapi."



    "Mimi nadhani, tukusanye hizi maiti tuzifiche mahala fulani. Kwanza naona bado dakika nne wale wapelelezi wa Ureno wafike hapa. Mimi naona tuwangojee hao hapa maana hawatakuwa na habari kuwa siye ndio tumo humu. Wakija tutawafungulia tukijifanya kama sisi ni walinzi wa Njoroge na kundi lake. Watakapokuwa wameingia ndipo sisi tuwageukie mbogo na kuwaua wote. Lakini lazima tuwe macho maana jua hawa watu pia ni wa kazi kama yetu kwa hiyo lazima wanaweza wakang'amua jambo fulani wakatuwahi kabla hatujawawahi. Pia lazima tuwe tunajua kuwa Benny na kundi lake wanaweza kurudi upesi iwezekanavyo kusudi waje wawazuie hawa watu, au awje na kundi la kuweza kutumalizia mbali. Lakini hii itamchukua muda mrefu kidogo hivyo tutaweza kupata nafasi ya kuwacheza hawa watu."



    Mawaidha ya Sammy niliyaona kuwa muruwa kabisa. Tulikusanya zile maiti na kuzitia kwenye chumba fulani. Halafu tukakaa tayari kuwangoja hao binadamu. Nilichukua bastola tatu toka kwa maiti hizo za kundi la Benny, na Sammy pia. Tukajitayarisha vizuri kabisa, maana mara hii tutapambana na watu waliofundishwa kazi hii hii kama sisi.



    Mlango uligongwa, miye nilienda kuufungua, Sammy alijificha kwenye chumba kimojawapo, "Come in, the boss is waiting for you," yaani"karibu ndani 'bosi'anawangojea."



    Thanks a lot ........" yaani" Asante sana, "walijibu. Walikuwa wavulana wanne na wasichana wawili, nilingoja wote waingie halafu mimi niwatokee kwa nyuma. Yule wa mwisho alipoingia, alitoa bastola mara moja na kuniuliza mahali alipo 'bosi'. Lo, nikaona hapa mambo yatachaga.



    Akaniambia nisitoe sauti, pia akaniuliza idadi ya walinzi wanaomlinda 'bosi'. Nikasema kumi na wanne. Akamweleza na mwenzake akamkubalia kuwa wanaweza kuwashinda tu, ila wakaambiana kuwa lazima wamgutushe 'bosi' na watu wake halafu wachukue hizo karatasi kwa nguvu kisha watoroke.



    Unaona sasa mambo yalivyokuwa yanachaga. Miye yaliyokuwa yananitisha sasa. Maana kumbe hawa watu hawakuja na fedha, ila tu walikuwa wamemfanyia 'bosi' akili, waje humu ndani kisha wawanyang'anye hizo karatasi kwa nguvu, halafu wawaue ndipo watoroke na hizo karatasi kwenda zao bila kulipa fedha hata senti moja.



    Alitaka kunipiga shingoni na kitako cha bastola, lakini kabla hajaniwahi miye nikakinga kwa mkono na ile bastola ikaruka. Hapo hapo nikatoa zangu vita ikaanza.



    Hawa wote sita walionekana watu wanaijua kazi yao barabara. Sammy alitokeza kwa nyuma kwa hiyo tukawaweka mahala pema sana. Fahamu mpaka sasa miye fulana yangu nilikuwa bado ninayo, kwa hiyo ilizidi kunisaidia sana. Mapigano kati yetu na kundi hili yalikuwa makali kupita mengine yote yaliyokuwa yameishapita. Mwishowe tulishinda, wanne wao tulikuwa tumeisha waua na wawili wengine walikuwa wamejeruhiwa vibaya sana.



    Tuliwaendea hawa waliojeruhiwa, wakatuuliza siye ni nani, tukawaeleza kila kitu. Nao wakatueleza kuwa kusema kweli nia yao haikuwa kulipa pesa zote hizo, maana serikali yao ni maskini sana kuweza kulipa pesa nyingi namna hiyo. Ila tu walikuwa wamemdanganya Njoroge na chama chake kusudi waweze kuzichukua hizo karatasi bila malipo yoyote.



    Sasa lililokuwa limebaki ni kupambana na Njoroge. Tuliona hii itakuwa kazi rahisi zaidi. "Miye Willy naona tungoje hapa maana Benny lazima atarudi, na mimi nataka nimwue Benny maana ndiye aliyemwua Robin, na mimi niliapa nitamwua mtu aliyemwua Robin asiponiua yeye," Alisema Sammy.



    "Vema, tutawangoja hapa."



    Kidogo tu, simu ililia. "Hallo, ni nani?" Nilijibu huku nikiuliza.



    "Sikiliza, njoni karibu na Railway Training School hapa Nairobi South, kuna nyumba moja mfano wa ghorofa chumba nambari saba. Hapa ndipo walipo kwa hiyo msikawie. Bado wanajaribu kukata shauri mahala pa kwenda. "Hii sauti ilikuwa kama ya mwanamke ingawaje ilibadilishwa na kusikika kama ya mwanaume. Tulikata shauri tufanye kama tulivyoambiwa.



    Tulienda mpaka karibu na RTS, halafu tukaanza kuitafuta ile nyumba, hii ilituchelewesha sana hata tukadhani tutakuta wameisha toka humo ndani. Mwishoni tukaiona, na hapo tukaenda ndani. Tukaenda mpaka chumba nambari saba. Tulipofika tukapiga mlango kwa nguvu, mpaka ndani.



    Nakwambia tulipoingia hatukuamini hata kidogo. Lulu alikuwa ameshikilia bastola mbili mkononi, Benny na 'bosi' wamekaa huku wameinua mikono juu.



    "Fanyeni haraka, wamemtuma mtu kuleta kundi jingine la watu. Watafika sasa hivi," alisema Lulu.



    "Hii ina maana gani Lulu," aliuliza Benny.



    "Mimi ni mpelelezi kutoka Uganda, ila nilifanya kazi nanyi nikijua tungeweza kuwashika vizuri sana. Tulikuwa na John katika kazi hii. Na ni John tu aliyekuwa akijua kazi yangu. Ulikuwa mpumbavu sana Benny uliponipenda sana. Nami niliwala akili vizuri sana hata wote mkaangukia upande wangu," alisema Lulu huku akimwemweseka.



    "Unaona sasa mjomba mambo yalivyozidi kunyumbulika. Kumbe Lulu alikuwa upande wetu. Kwanza siku ile Benny alipotaka kutuchoma na petrol, Lulu alisema wamwendee 'bosi', huku akaponya maisha yetu. Kadhalika na kule chumbani 'Wilson Airport' aliniangushia bastola. Halafu nikiwaambia wasichana ni sumu nyie mnanidhania mimi ni mpumbavu ........."



    "Wapi karatasi?" Nilimuuliza Daktari Njoroge.



    "Zipo hapa," alizitoa huku akitetemeka.



    "Wale Wareno wote tumeisha waua, lakini kabla hujafa nitakueleza kuwa uhalifu haulipi hata kidogo. Wale watu nao walikuwa wamekuzunguka. Nia yao ilikuwa kukunyang'anya hizo karatasi kwa nguvu, halafu wakuue, unaona hiyo," nilimweleza huku nikienda kuzichukua hizo karatasi. Niliziangalia nikahakikisha kuwa kweli zilikuwa zenyewe.



    Hatukutaka kupoteza wakati kwani tulihofia kukutwa na hilo kundi jingine la wahalifu hawa. Hivyo haraka tukapiga simu polisi. Si baadaye motakaa ya polisi ilisimama nje ya jumba hili tulimokuwa, punde askari polisi kadhaa wakaingia tulipokuwa. Nyuso zao ziliainisha ghadhabu iliyokithiri kiwango. Haikosi kila mmoja wao alichukizwa sana na hila za wasaliti hawa ambao ati ni pamoja na wazalendo wa Afrika!



    Moyo wangu ulirudi kwa Lina. Kama mwehu, nikawaacha wote na kutia gari moto kwenda kumwona Lina maana mpaka sasa moyo wangu ulikuwa bado ukiniuma kwa ajili yake.



    Nilipofika kwa daktari nilingia kwa fujo sana maana nilikuwa na hamu ya kutaka kusikia nini kimempata Lina.



    "Daktari, Lina vipi?"



    "Naona ataishi, ila kwa sasa usiende kumwona maana unaweza kumsumbua,"



    "Hata, lazima nimwone, nisipomwona naweza kuzimia,"



    "Hapana usiende kumwona tafadhali."



    "Nyamaza daktari." Nilimvuta daktari mkono. Akaona hana la kufanya ila kufanya kama ninavyomwambia.



    Nilipoingia Lina alikuwa amesinzia. Nilimwinamia na kuanza kumbusu ovyo. Daktari alicheka akasema. "Naona kweli mapenzi ni hatari-yaweza kuua." Akafunga mlango akaenda zake. Lina alifungua macho yake.



    "Oh Willy, nilikuwa nakuota sasa hivi umenikumbatia, kumbe ni kweli. Oh, sasa nimepona kabisa, nibusu Willy nikarejewe na uhai."



    "Lina, Lina mpenzi, mimi na wewe mpaka kwa mama Willy kifo ndicho kitakacho tutenganisha."

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    MWISHO


0 comments:

Post a Comment

Blog