Search This Blog

Saturday 5 November 2022

MAGNUM 22 - 1

 




IMEANDIKWA NA : RICHARD MWAMBE



*********************************************************************************



Simulizi : Magnum 22

Sehemu Ya Kwanza (1)



SEHEMU FULANI HUKO AFRIKA MAGAHARIBI

MACHO YANGU yalikuwa mazito sana kiasi kwamba iliniwia ngumu kuyafumbua. Haikuwa rahisi kwangu, nilijaribu kutumia nguvu ya mwisho niliyonayo kuona japo nuru, haikuwezekana. Fahamu zilipokaa sawa nikahisi maumivu makali sana kisogoni, nikajaribu kuinua mkono ili japo kushika eneo hilo la mwili. Damu! Damu iliyoanza kuganda na kufanya kama buja zito iligandamana na nywele zangu, nilipopapasa zaidi nikagundua kuwa nina mpasuko au niite mchaniko.

Bado giza nene liliyafanya macho yangu yashindwe kuona chochote, mboni zilifunguka na kufunguka lakini kuiona nuru ilikuwa ndoto.

Niko wapi? Nikajiuliza, hakukuwa na wa kunijibu zaidi ya mvumo wa giza kuyapa taabu masikio yangu. Maumivu ya jeraha langu la kisogoni yakaanza kuhisika kwa mbali, nikahisi kama moyo umehamia hapo kwa jinsi ulivyokuwa ukipwita. Kila nukta ya sekunde iliyopita, maumivu yake yalizidi nikaanza kuhisi kero, nikajaribu kujigeuza, kichwa kizito, nilipotumia nguvu zote kujigeuza nikahisi kugonga vitu vigumu kama kuni zilizorundikwa lakini kwa mpangilio maalumu. Nikatulia kwa sekunde chache huku nikijaribu kuvuta hisia kutambua ni nini nimekigonga. Nikainua mkono na kupapasa, sikujua kama nimeshika fimbo au kota la kutungulia embe. Nikapapasa ka sentimeta kadhaa, mara nikahisi kitu ambacho sikukitegemea, mwisho wa kile nilichokipapasa nikahisi nimeshika kitanga cha mkono wa mwanadamu, nikakipapasa vyema nikajiridhisha kuwa ndiyo ni kitanga cha mkono lakini kimebaki mifupa tupu.

Nikachezesha mguu wangu nao ukagonga vitu vingine kama hivyo, ndipo nikagundua kuwa hata maumivu mengine ninayoyasikia ni kwa sababu nimelalia mifupa ya binadamu iliyojaa katika eneo hilo.

“Shiiiit!!!!” nikang’aka kwa sauti, kisha nikajiinua kuketi, kiuno changu nacho kikagosha kwa nguvu. Hapo nikagundua kuwa hta kiuno nacho kimepata tabu kidogo. Nikavumilia na kufanikiwa kuketi, kila nilipogusa na kushika kulikuwa na mifupa tu, mafuvu nayo niliyapapasa kama vifuu vya nazi. Sikuweza kuona kwa macho yangu kutokana na giza nene katika eneo hilo. Kila sekunde iliyopita nilizidi kuipata hali halisi ya ndani humo, harufu ya mauti ilitapakaa.

Wakiua huwa wanatupa maiti humu! Nikawaza.

Ina maana hata mimi walijua nimekufa? Nikajiuliza. Zaidi ya hapo sikuwa na lingine la kufanya zaidi ya kuutafuta kama ni ukuta au ni kitu gani kinachofanya miimo ya eneo hilo. Maumivu yalinizidi katika kisogo change kiasi kwamba iliniwia ngumu kuvumilia. Nikatambaa kwa shida nikiparamia mifupa na skeleton za binadamu, na kwa sababu nilikuwa sioni niendako nikajikuta na jigonga kwenye ukuta. Nikatulia na kuanza kuupapasa huku nikiugulia kwa maumivu. Ukuta ulikuwa laini na wa kutereza, wenye vitu kama marumaru kwa jinsi vilivyounganishwa, nikaupapasa na kufanikiwa kusimama lakini sikufikia juu, parefu.

Kaburi! Nikawaza na hapo nikaanza kupata kizunguzungu kwa sababu sikuwahi kuingia kaburini tangu nizaliwe, lakini mara hii nimezikwa mzima mzima? Nikajikuta naanguka kwa nguvu na kufikia juu ya miili iliyooza zamani maumivu yake hasa sehemu za kisogo changu yalizidi lakini nikazidi kuidhihirishia hali hiyo kuwa mimi ni mwanaume.

“Chwaaaa!!!! Chwaaaa!!!!” nikasikia mtu akipiga chafya, hii sasa ikanifanya nishikwe na hofu kuu. Pamoja na ukakamavu wangu na ujuvi wa upiganaji na kujilinda, nilijikuta Napata woga wa ajabu uliotiririka kutoka utosini mpaka unyayoni, moyo wangu ulikwenda mpio kama saa mbovu, macho ya kanitoka pima maana sikujua kama ni maiti imepata uhai, au ndiyo moja ya vitisho vya humu ndani au inakuaje, maana kwa mtindo huu mtu unaweza kufa kihoro. Tatizo kubwa sikuwa namwona mtu huyo au kiumbe hicho maana giza lilikuwa nene sana, joto nalo lilikuwa kali mno, nikajiinua na kutafuta kona ya ukuta huo kwa taabu nikaipata na kujiegama hapo nikisubiri hatima yangu.

“Kheeeee!!!!!” ile sauti ikakoroma, nikajiweka sawa, sasa nilijua nipo kwenye kona ya kaburi hilo, hata kama nitashambuliwa, basi shambulizi litatoka ndani ya nyuzi arobaini na tano tu, ningeweza kukabiliana nalo hata kama ni giza. Nilianza kuvuta hisia ambazo nilifundishwa na Master wangu wakati nipo Japan kwenye mafunzo magumu sana ya Karate huku nikiwa nimefungwa kitambaa usoni, jinsi ya kumhisi adui yuko upande gani, kusikiliza mgongano wa hewa na kujua adui anatumia pigo gani, kumwona adui ndani ya hisia ya sita.

“Chwaaaa! Khaaaaa!!!!” chafya nikasisikia tena na mkhoromo ukafuatia, safari hii sikuogopa, ila nilikuwa nimelowa jasho na hewa nzito ndani humo ilianza kunishinda taratibu na kujihisi kuchoka. Njaa nayo ikaendelea kuleta upinzani mkubwa. Mara ule mkhoromo ukaendelea sasa ukaanza kuyasumbua masikio yangu, nikagundua huyo ni mwanadamu ambaye amefika dakika za mwisho za uhai wake.

Anakufa? Nikajiuliza, kwa kuwa nilishajua ni upande gani alipo huyo akoromaye, nikainuka haraka na kaukanyaga mifupa na miili mikavu mpaka pale nilipohisi, naam ndipo. Nikajikuta nimepiga magoti na kuanza kumtikisa huyo mtu, mikono yangu nikahisi imeshika kitu kama koti la suti, nikamtikisa na kumtikisa, yeye akazidi kukoroma tu. Nikampapasa usoni nikahisi kuwa ana majeraha mengi na ya kutisha kani nilihisi nashika mtu asiye na macho. Yule mtu aliye kufani akanishika mkono kwa nguvu zake zote na kuupachika katika mkanda wa suruali yake kisha yeye mwenyewe akatulia kimya kabisa, mkono wake ukalegea, nikajua tayari andipela.

Hapo nikajikuta kwenye hofu kuu, hofu ya kifo, nikajikuta nimesahahu mateso yangu yote, na mawazo yangu yakawa juu ya mtu huyo. Akili iliporudi, nikaanza kumsachi kuanzia mifuko ya koti, shati lake na suruali. Katika mfuko wa ndani wa shati nikatoa kijitabu kidogo sana, sikuweza kukisoma kwani hapa nilikuwa natumia hisia tu kutambua vitu, katika viatu vyake baada ya kumvua nikatoa karatasi ambayo sikuweza kujua ni karatasi ya nini au gani. Nikakumbuka kuwa mtu huyu alipoushika mkono wangu kwa nguvu aliuweka kwenye mkanda wa kiunoni.

Inawezekana kuna ujumbe katika mkanda huo! Nikawaza na kuanza kuufungua kiunoni mwake nikautoa na kuushika mkononi. Ni mkanda tu wa ngozi wenye chuma kikubwa cha kuufungia kutoka upande huu kwenda huu.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Ujumbe gani upon a mkanda huu? Nikajiuliza, sikuwa na jibu, ambaye ningemuuliza, ameshakufa, sasa nafanyaje. Maumivu niliyoyasahau ghafla nikaanza kuyahisi upya kwa nguvu, joto kali, shati lote likawa chapachapa kwa jasho na suruali pia ikaanza kuwa katika hali hiyo. Nikatia kile kijitabu mfukoni na ile karatasi.

Vitanisaidia nini sasa, labda kama ningepata nuru ya kusoma au kuona ni vitu gani… nikajiambia kwa sauti ya moyoni kisha nikajiegemeza katika ukuta upande mwingine. Hapo nikahisi naishiwa nguvu kabisa, pumzi nazipata kwa taabu sana nikajua sasa muda wangu umekwisha, nikafunga mikono na kuanza kusali sala zangu za mwisho. Nikaomba kwa Mungu wangu, msamaha kwa yote niliyoyakosa, lakini nikamwachia kila kitu aamue yeye kwani yeye anajua kuwa yepi nimeyafanya kimakosa na yepi nilikuwa kazini. Japokuwa sikuwa nawaona wengine, kupitia sala zangu hizi nikawaomba msamaha wote.

Joto lilizidi kuwa kali, harufu nzito ya mauti ikaanza kuzisumbua upya pua zangu, giza nalo likawa adui mkubwa. Nikatulia kimya nikiwa nimejikunyata huku mikononi nikiwa nimeukamata mkanda wa yule marehemu aliyenitangulia. Kutoka moyoni nikahisi sauti ikinitaka kuufunga mkanda ule kiunoni, nikaipuuzia lakini baadae ikazidi kunisumbua, nikaamua kuitii hisia hii kwani ni moja ya kazi yetu kutii hisia ya sita na ndiyo intelijensia yenyewe. Nilikuwa naishiwa nguvu, nikaupachika kiunoni tu bila kuuweka kwenye lupsi za suruali kwani sikuwa na muda na nguvu hizo. Nikachuku mwisho huu na huu na kuukutanisha kisha nikaupachika kwa nguvu ili meno yake yaumane. Sekunde ileile nilipoupachika na yale meno kuumana, nikasikia mlipuko kutoka upande mmoja wa ukuta, vumbi likatawala ndani ya kaburi hilo, nikakohoa kwa nguvu sana, hali ilipotulia nikaona tundu la ukubwa wa mdomo wa pipa katika ukuta wa kushoto kwangu. Mwanga hafifu ukapenya ndani nikajua kuwa kwa hapo ningeweza





kujiokoa, sasa ndani humu kulikuwa na mwanga ambao haukuweza kunionesha kila kilichomo bali angalau nilijuwa kuwa ukuta ni wa marumaru nyeupe kama za chooni, kwa shida niliona kweli miili mingi iliyokauka na mifupa isiyohesabika, sikuijali bali nilijijali mwenyewe kwa wakati huo. Nikajivuta mpaka kwenye lile tundu, lilikuwa refu kwenda chini. Na chini kabisa lilionekana kuelekea upande mwingine.

Ina maana hapa nipo juu au wapi? Nikajiuliza na kisha nikakamata bomba moja ndani ya mfereji au bomba hilo nikajitoa na kujitumbukiza, bahati mbaya lile bomba halikuwa na imara likakatika.

“Aaaaaaaaiiiiiiigggghhhhh!!!!” nikajikuta napiga kelele, nikajibamiza katika kuta za shimo hilo na kujigonga vibaya kisogoni. Giza kuu likanifunika, huku nikihisi upepo mkali ukipita masikioni mwangu kisha ukimya mkuu ukanitawala.







SHAMBA – SAFE HOUSE

HALI YA SINTOFAHAMU ilitanda ndani ya afisi hii ya siri, kila mmoja kichwani alikuwa anawaza lake, hakuna aliyekuwa akiongea na mwenzake. Meza, ambayo daima huwa imejawa na watu hawa sita leo ilikuwa tupu, ni taa inayoning’inia juu yake na makabrasha kadhaa ndivyo vilibakia mezani hapo, hakukuwa na mtu. Katika chumba kimojawapo ndani ya jengo hilo, Madam S alikuwa ameketi kimya kabisa, peke yake, meza ilikuwa na kabrasha moja tu na kiti cha mbele yake hakikuwa na mtu yeyote. Kalamu ilikuwa ikizungushwa katika vidole vya mikono yake huku macho yake yakiwa yamefumbwa kwa utulivu. Mwanamama huyu, mzoefu katika maswala ya intelijensia hupenda kujifungia ndani ya chumba hiki pindi mambo yakiwa magumu. Nywele zake zilionekana wazi kujawa mvi chwe! Ngozi ya uso wake nayo ilionesha wazi kuwa uzee umebisha hodi, kama si pesa basi tayari tungemwita mzee ila kwa sasa tumwite ‘mama mtu mzima’, alijua kujitunza.

Akiwa katika ukimya huo akagutushwa na simu iliyokuwa ikiunguruma kwa fujo kwenye meza yake, akainyakuwa na kuitazama kwenye kioo.

‘Unknown Caller ID’

Ilijiandika namna hiyo, kabla hajaipokea akatuliza moyo kwanza maana ulikuwa ukienda mbiyo. Simu hii ni ile ambayo huwa haipigwi ovyo, ni watu wachache sana hupiga, lakini kila apigaye namba yake huonekana, ni mara hii tu ilijiandika neno hili. Akabonya kitufe fulani pembeni ya simu hiyo na kisha akaiweka sikioni, bila kuongea.

“Selina!” upande wa pili ukaita, kwa sauti hiyo tu akatambua kuwa anayepiga si mwingine ni Inspekta Simbeye.

“Mzee vipi? Mbona unaniweka roho juu kwa kuficha ID yako?” akamuuliza.

“Oh sorry!”

“Enhe nambie…. Kuna lingine mtaani?” Madam S akauliza.

“Hakuna lingine, nilitaka kujua kama umepata lolote kuhusu kazi yetu,” Simbeye akamwambia Madam S.

“Hapana! Bado tumechanganyikiwa, ni saa la 120 sasa hatujajua kinachoendelea,” Madam S akajibu.

“Nimepata ujumbe mwingine hapa…”

“Unasemaje…”

“Ataendelea kuua viongozi wa Afrika mpaka AU isalimu amri,”

“Kichaa… kichaa! Si bure… bado tunamfanyia kazi tutamnasa tu!” akaongea kwa jazba huku mwili wake ukitetemeka kwa mbali.

“Kwa lolote tutakuwa tukiwasiliana,” Inspekta Simbeye kutakamaliza na kukata simu. Madam S hakukata simu haraka badala yake akasubiri kidogo na hapo akasikia ‘kliki’ nyingine mbili za kukata simu hiyo. Hapo Madam akaju moja kwa moja kuwa simu hiyo imesikilizwa na watu wawili zaidi yake, ni akina nani hao? Akatoka ndani ya chumba hicho na kuelekea kile cha mawasiliano ambako alimkuta Chiba na Jasmini wakiwa wametingwa na kufanya hili na lile kwenye kompyuta ndani ya chumba hicho.

“Chiba!” akaita.

“Yes Mom!” Kijana huyo akaitika na kuacha kile alichokuwa akifanya.

“Umesikiliza simu niliyokuwa napigiwa sasa hivi?” akamuuliza.

“Yes, na nimeirekodi, nimekosea?” akauliza.

“Hujakosea, vipi hujagundua uwa simu hiyo imesikilizwa na watu watatu yaani mimi, wewe na mwingine zaidi?” Madam akauliza.

“Hapana!”

“Usiwe unawahi kukata simu, daima subiri sekunde kadhaa baada ya mpigaji kukata unaweza kugundua kuwa kuna mwingine anakusikiliza…” akamwambia.

“Shiiiit! So?”

“Hatuna budi kumtracy!”

“Sawa mama!” Chiba akajibu na kurudi kitini tena.

Madam S kutoka pale aliposimama, akavuta hatua na kuingia ndani kabisa ya chumba hicho, akavuta kiti cha akiba kilichokuwapo, akaketi.

“Gina yuko wapi?” akauliza.

“Ametoka, kaenda Uwanja wa ndege mara moja,” Jasmini akawa wa kwanza kujibu.

“Kuna la maana huko?”

“Aaaaannn naweza kusema yes au no ila ni maswala ya kikazi,” Jasmini akajibu tena.

“Ok! Tetesi yoyote Chiba…”

“Hakuna tetesi mama, nimejaribu mbinu zote nimeshindwa kumpata alipo, sipati signal ya GPS wala nini, hakuna kitu na sasa ni siku ya tano, huwa si kawaida….”

“Inamaanisha…”

“Man Down!” Chiba akamalizia.

“No! napingana na mawazo hayo, kinadharia ndiyo, ila kiuhalisia najua yule mwanaume ni mjanja anaweza akafufuka hata baada ya siku kumi, naomba tusiamini mpaka tutakapoupata mwili wake,” Madam akawaambia na kusimama.

“Call ya mwisho alikwambia nini na alikuwa wapi?” Madam akamuuliza.

“Alikuwa Freetown, na aliafikia katika hoteli ya kawaida sana ya Swiss Spirit,” Chiba akamwambia Madam.

“Inabidi kwenda kufuatilia Chiba, jiandae…” Madam akamwambia kijana wake.

“Mimi?”

“Ndiyo, wewe si ndiyo TSA 2?” Madam akamwambia huku akikiacha chumba kile.

“Come on!” Chiba akapiga kite na kuinuka, moja kwa moja akaingia chumba cha mazoezi na kuvua suruali yake na shati akavaa Karategi lake na kuanza mazoenzi makali kama kichaa. Alikuwa akijikunja na kupiga mapigo ya hatari huku akitoa kelele zenye mirindimo tofauti.

* * *

OFISI ZA MUDA ZA USALAMA ZA AU

Madam S alikunja kona kutoka barabara ya Haile Selassie na kuingi ile ndogo ya Ruvu, mwendo kama wa mita hamsini hivi akakunja kushoto na kuingia moja kwa moja kwenye geti lililokuwa wazi. Akaegesha gari katikati ya magari mengine ambayo yalikuwa hapo, akashuka na kuufunga mlango. Hatua zake fupifupi zikamfikisha kwenye mlango wa kawaida tu, akausukuma na kuingia ndani, hapo akakutana na mwanadada mrembo aliyekuwa nyuma ya kompyuta akiendelea na kazi.

Baada ya kusalimiana, mwanadada huyo akamwongoza mgeni mpaka chumba namba tano.

“Ni wewe tu unasubiriwa!” yule mwanadada akamwambia huku akimfungulia mlango na Madam S akaingia na kuchukua kiti chake. Ulikuwa ukumbi mdogo wenye viti sita na kati ya viti hivyo palikuwa na meza kubwa yenye umbo la yai. Nyumba hii iliyo chini ya Shirika la Nyumba la Taifa ilibadilishwa matumizi ghafla baada ya mkutano wa Baraza la Usalama la nchi huru za Afrika kuamua iwe hivyo kufuatia matukio ya kutisha yaliyokuwa yakiwakumba viongozi wan chi hizo katika maeneo tofauti ya bara hilo. Baraza la usalama katika kikao chake cha mwisho likaiomba Tanzania kuiweka ofisi hiyo nchini kwake kwa muda mpaka tatizo hilo litakapopatiwa ufumbuzi.

“Karibu sana Sellina!” Rais wa baraza hilo alimkaribisha.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Asante nimefika!” akajibu na kuketi.

Kilikuwa ni kikao cha watu sita tu, na Madam S alikuwa ni mwanamama pekee katika jopo hili la wanaintelijensia hatari wa Afrika ambao kila mmoja kama si kustaafu basi alikuwa akiendesha Secret Services katika taifa lake kama ilivyo kwa Madam S.

“Karibuni wajumbe! Naomba kila mmoja afungue kabrasha lake na kupitia kilichomo humo ndani…” Rais wa baraza hilo ambaye pia aliteuliwa kama mwenyekiti wa tume hiyo ya usalama aliwataka wajumbe kufanya hivyo. Kila mmoja alichukua kama dakika kumi hivi kusoma kabrasha lake kisha wakafunga kwa nyakati tofauti.

“Ina maana haya mauaji yanaendeshwa na kikundi hiki au na mtu huyu?” Madam S akawa wa kwanza kuuliza.

“Ndiyo!” akajibiwa.

“Sasa kama mpaka picha yake tunayo tunashndwa nini kumkamata au kumuulia mbali?” akauliza tena.

“Swali zuri, baada ya uchunguzi wa awali kufanyika huyu amekuwa mtuhumiwa wa kwanza anaitwa Bwana Fadicky Al Habib, picha hii ilipigwa Mogadishu na askari wa jeshi la kulinda amani la AU baada ya kumshuku kutokana na mzungumzo yake…”

“Sina uhakika mwenyekiti,” Madam S akapinga, “kwanza tuangalie chanzo hasa cha mauaji haya na kwa nini yanafanyika, pia tutazama ujumbe ambao muuaji amekuwa akituma siku au saa chache kabla ya kutekeleza takwa lake…” akaunguruma na wanaume wote ndani ya kikao hicho wakabaki kimya.

“Hatutakiwi kuchukulia mambo haya kirahisi namna hii, maadam mmetaka taasisi ya intelijensi ya Tanzania ifanye kazi basi naomba msipokee taarifa nyingine kutoka upande wowote wa dunia, unless otherwise tutakuwa tunayumbishwa na kila anayetaka kufanya hivyo…” Madam S akaendelea.

“Cool down Madam Seline Mwenyekiti akamwambia na wajumbe wengine wakatikisa vichwa kukubali, “ipo hivi, katika siku saba hizi ambazo hatujapata taarifa yoyote kutoka kwako, utaratibu wa siri ulifanyika na ndipo tukapata taarifa hii, hivyo hatuna budi kufanyia kazi hii na siyo nyingine yoyote. Kumbuka kikao chetu cha mwisho tulikubaliana kuwa kila siku tatu tupeane taarifa, lakini mpaka sasa hatujapata zaidi ya zile tatu za kwanza…” Mwenyekiti akasema na kutulia kidogo.

“Naunga mkono asemalo mwenyekiti, mi’ nafikiri kama tulivyofikiri, tuunde timu nyingine ya wapelelezi watakaofikisha suala hili mwisho, maana wapelelezi wa Tanzania wapo kimya…”

“Si kwamba tupo kimya, tunafanya kazi, na hizi taarifa si ‘confidencial’, wala si ‘secret’ bali ni ‘top secret’ hivyo hatuwezi kuzitoa ovyo isipokuwa kwa mtu mmoja tu, sasa tunaziweka pamoja na mtazipata as soon as possible!” Madam S akaliambia jopo la watu hao kutoka nchi tofauti za Afrika.

Ukimya ukatawala kwa nukta kadhaa kati ya wote sita, baadae kidogo mwenyekiti wa kikao hicho ambaye ndiye rais wa Baraza la Usalama la AU akajikohoza na kuuvunja ukimya huo.

“Kwa hiyo unataka kutuambiaje?” akamuuliza mwanamke huyo.

“Mtapata taarifa kwani tumefikia hatua nzuri tu…”

“…No! imetosha, lazima tuunde jopo lingine la kufanya upelelezi huu…”

“Sawa, undeni, ni sawa tu! Maadam hata sisi kiongozi wetu mmoja ameuawa na watu hao, tutafanya upelelezi kama serikali kumsaka muuaji na ninyi muendelee, asante!” Madam S akazungumza huku amesimama, akafunga kabrasha lake na kuliinua tayari kwa safari.

“Unaenda wapi?” Mwenyekiti akamzuia.

“Kikao hakina maana kwangu, wacha niende nanyi muendelee na kazi yenu, mkiihitaji msaada mtatutafuta,” akamjibu.

“Kwa hiyo umesusa?” Mkuu wa idara ya usalama wa taifa ya Afrika Kusini akauliza.

“Yes! Naenda kuabort mission, hata nikikaa hapa nina machango gani?”

“Tunakuhitaji wewe, ila hatuihitaji timu yako…”

“Impossible!!!” akajibu kwa neno moja tu.

“Kaa chini, kikao kiingie awamu ya pili,” Mwenyekiti akaamuru.

“Awamu ya pili!” Madam akashangaa.

“Yes! Awamu ya pili, kuunda kikosi kazi kingine…” Mwenyekiti akajibu.

Kikao kile kikaingia awamu ya pili kama ilivyotamkwa na katika hii ajenda ilikuwa ni kuunda kikosi kipya cha upelelezi kitakachofanya kazi zake moja kwa moja chini ya baraza hili. Wapelelezi mashuhuri kadhaa kutoka nchi za Maghalibi na Kasakzini na Kusini wakawekwa pamoja, wengine hata walikuwa tayari wamestahafu, lakini kwa hili wakatakiwa kurudi kazini mara moja. Watu hao kwa idadi walikuwa watano wakatakiwa kufika Dar es salaam mara moja kila mtu kwa wakati wake na kupangiwa kazi.

“Nataka tukomeshe kabisa uhuni huu, tumeshapoteza viongozi watatu wakubwa Afrika ndani ya miezi sita, hatutaki hali hii iendelee hata kidogo, yoyote anayehusika ashughurikiwe tukianza na huyu kwenye hii picha!” Mwenyekiti akaliambia jopo baada ya kuwa tayari kikosi kimepatikana. Madam S akabaki kimya, hakutaka hata kuchangia neno kwa jinsi alivyoshikwa na hasira na maamuzi hayo. Hasira yake ilikuja mara mbili; kwanza kwa kusitisha operesheni nyingine, na pili mpaka dakika hiyo bado hajui kijana wake yuko wapi na katika hali gani.

“Selina unasemaje katika hilo?” Mwenyekiti akauliza baada ya kuwauliza wengine wote.

“Naunga mkono hoja!” akajibu.





Baada ya mazungumzo marefu, kikao kikafungwa na wajumbe wakatawanyika kwa miadi ya kukutana kesho yake ambapo mtu wa kwanza atakuwa amewasili kwa ajili ya kugewa majukumu yake.

Mara baada ya kumalza kikao hicho, Madam S alikanyaga mafuta moja kwa moja mpaka makazi binafsi ya Mheshimiwa Rais huko Oysterbay. Alipowasili tu, akafunguliwa geti na kuingia mpaka maegeshoni ambako alimkuta Rais akimsubiri hapo.

“Karibu sana Selina!” akamkaribisha huku akimfungulia mlango wa gari hilo.

“Asante,”

“Kikao kimekwenda vizuri?”

“Hapana kwa sababu wametaka tuabbort mission, wameunda kikosi kingine kwa ajili ya kazi hii,” Madam akajibu.

“Mmmmhhh!!! Ina maana hawana imani na sisi?” akauliza tena.

“Hawana imani, wanasema hatujawapa majibu kwa siku tatu hizi, so hawajui nini kinaendelea, ukimya umewafanya wao wajue tumeshindwa. Wanasema una mmoja wa vijana wao wa siri kawatumia picha hii na kumhisi mtu huyu kuwa ndiye mhusika wa mambo haya,” akamwambia huku akimpa ile bahasha. Mheshimiwa Rais, akaitazama ile picha kwa makini sana.

“Anaitwa Fadicky Al-Habib,” Madam S akamtajia jina hilo.

“Kwa hiyo tunasitisha operesheni?” akauliza.

“Kamwe! Kwanza mpaka sasa kijana wangu sijajua nini kimempata maana sina mawasiliano naye, hatuwezi kusitisha zoezi kwa sababu tumefika mahali pazuri sana katika upelelezi huu…” akaeleza.

“Ulimtuma nani kule?”

“Namba moja!” akashangaa. Ilimchukua kama sekunde kumi na tano akili kumkaa sawa, akamshika bega Madam S na kuingia ndani katika varanda ndogo, akamkaribisha kiti na kuletewa kinywaji kikali, akaamuru walinzi watoke na yeye abaki na Madam S pekee.

“Unataka kunambia kuna habari mbaya kwa TSA 1?” akauliza.

“Bado hatujafikia kusema hivyo, na tunaamini kuwa anaweza kufanya lolote huko aliko,” Madam akamjibu, “hata hivyo kesho TSA 2 ataondoka kuelekea Sierra Leone kwa ajili ya kumtafuta mwenzake…”

“Come on!” Mheshimiwa akatulia kwa nukta kadhaa, akainua bilauri na kupiga mafunda kadhaa ya kinywaji, kisha akaitua, “hakikisha habari zote unanipatia, kama unavyojua, idara yako ni kama moyo wa Ikulu na utendaji mzima wa Rais, kama kunahitajika msaada wowote, fanay kama ufanyavyo kawaida,” akamaliza na kuagana na mwanamke huyo. Walinzi wa Rais daima walimwona mwanamke huyu mara kwa mara akija na kila alipotaka kuzungumza naye faragha aliwaondsha; wapo walioamini kuwa ni demu wake, wapo waliojua kuwa alikuwa ni classmate na mengine mengi, lakini hawakuwahi kujua kama ana cheo kikubwa katika idara nyeti ya usalama wa taifa hili.

* * *

KITONGOJI CHA WATERLOO

SIERRA LEONE

MARTIN Gupter akafunga pazia la dirisha na kurudi tena mezani ambapo aliwaacha wenzake.

“Vipi?” mwanamke pekee katika jopo hilo akamtupia swali.

“Ni yeye! Anapita na watu wake, anajivunia kuukwaa urais wa nchi hii…” Martin akamjibu huku akiketi tena mahala pake.

“Wamempa tu, si swahiba wao, lakini wataona kile ambacho tutakifanya, safari hii lazima niishangaze Afrika kama nilichokifanya pale Lusaka! Na watasaka mpaka wakome hawatanipata…” Yule mwanamke aliyejulikana kama Amanda akawaambia wenzake.

“Mpango upoje?” kijana mwingine akauliza.

“Kama kawaida, ni keshokutwa tu, lazima tuangushe wa nne, hii itawapa kiwewe, watakubali tu tunachotaka,” yule mwanamke akajibu huku akismama.

“Kama kuna mpelelezi ambaye nilikwishapewa jina lake kuwa ni wakumwogopa ndiye huyo tayari yupo kwenye kaburi la halaiki, hajawahi kutoka mtu mle…”

“Zaidi ya hapo hakuna mwingine… hawa wengine watoto tu,” Frederick Garincha, kijana mpole asiye na mawaa akawaambia wenzake.

“Timu imetimia hatujawahi kuharibu, na hatutaharibu kamwe…”

Vijana hawa watatu ndani ya nyumba hii kubwa ya ghorofa walikuwa wamepiga kambi kwa muda, mambo yao na mipango yao ilikuwa ikipangwa kwenye majumba ya siri ambayo yalitapakaa miji tafauti Afrika. Walikuwa wamebobea kwenye kazi mbalimbali za kigaidi, mauaji, wizi na kadhalika, mara hii walikuwa wamepata kazi katika Bara la Afrika. Mkataba mnono, wenye pesa za kutosha, hawakukataa bali waliifanya kazi hiyo kwa umakini usioelezeka. Afrika ilihaha pale Rais wa nchi ya Angola alipotunguliwa kwa risasi akiwa katika gari lake. Liikuwa ni tukio ambalo wanausalama hawakulitegemea kabisa, na baada ya hapo hawakufanikiwa kumpata muuaji wala nyayo zake.



…MIEZI SITA ILIYOPITA

LUANDA – ANGOLA

ASUBUHI ya siku hii kulikuwa na hali ya mawingu kiasi, ukizingatia ni mwisho wa juma hakukuwa na kashkash za wapita njia kama ilivyo siku za kazi. Utulivu ulishika hatamu kila kiunga cha jiji hilo, zaidi ya wafanya biashara kufungua maduka ni watu wachache sana walioonekana kwenda huku na kule hasa akinamama kwa kuwa walihitaji chochote kwa siku hiyo, wao na familia zao.

Askari maalumu wa usalama barabarani katika jiji hilo walianza kuonekana kwenye barabara nyeti ambayo kiongozi wa nchi huitumia mara nyingi kutoka makao yake kuelekea Uwanja wa ndege kama anakuwa na safari ya kutumia usafiri wa anga. Hakuna aliyekuwa anajua nini ambacho kitatukia siku hiyo na kuitikisa nchi hiyo kwa mapana na marefu. Watu wenye fikra mbili tofauti walikuwa ndani ya jiji moja. Upande huu wanausalama walioakikisha Rais na watu wake wanakuwa salama muda wote katika safari hiyo walikuwa wanawasiliana kujiridhisha hali halisi ya siku hiyo. Mambo kadhaa yalikuwa yakiwekwa sawa, huwa tunaita itifaki, barabara ya kupitia msafar huo tayari ilikuwa chini ya ulinzi mkali, ikiwa imeshafungwa mitambo yote kuhakikisha usalama. Katika jiji hilohilo kulikuwa na kundi lingine la watu watatu nao walikuwa wakiweka mambo sawa kwa upande wa kazi yake. Hawa hawakuwa wengine zaidi ya Amanda Keller, Martin Gupter na Frederick Garincha. Jamaa hawa waliingia nchini humo kwa usafiri wa barabara wakitokea nchi ya Jamhuri ya Congo yaani Zaire ya zamani.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Kadiri ya mipango yao hawakutaka kuingia nchini humo kwa ndege kwani ingeweza kuhatarisha usalma wao. Ni Amanda pekee aliyeingie kwa njia hiyo kwa kuwa alitakiwa kuwahi angalau juma moaj kabla ili kuweza kufanya udukuzi wa mipango na maisha ya mheshimiwa ili kujua ni jinsi gani wataweza kufanikisha azma ya mteja wao.

Ndani ya jumba hili kubwa wawili yaani Frederick na Martin walikuwa tayari kwa kazi asubuhi hii wakati Amanda akiwa nje akifanya mazoezi ya kukimbia. Kiujumla haikuwa mazoezi kama mazoezi bali ni moja ya kukusanya taarifa kama watu wa usalama wamegundua chochote katika njama hiyo.

Martin Gupter aliijua vyema kazi yake, aliitazama saa yake ya mkononi na mara moja akaliendea dirisha la upande wa barabara kuu ya Avenue Revolucao de Outubro ambayo inaelekea moja kwa moja katika Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Quatro de Fevereiro. Mbinu chafu iliyofanywa na Amanda ni kupandikiza kifaa cha mawasiliano kwa mmoja wa watu wa usalama waliokuwa barabarani huko nje alipojifanya ameumia na kijana huyo kutaka kumsaidia.

“Time is now!” Frederick alimwambia Martin na wawili hao wakagawana. Fred akateremka chini kutoka ghorofani na kuingia garini huku akimwacha Martin kijana wa Ki-Holland akiwa tayari kweka bunduki yake kwa kificho dirishani na jicho lake likiwa kwenye lensi iliyofungwa vyema juu ya bunduki hiyo ya kawaida kabisa.

Alipojiridhisha, akaikunja katikati na kuchukua risasi moja tu, kubwa yeney nguvu, akaitumbukiza mahala pake na kuirudishia bunduki hiyo kama kwanza, akaipachika tena kwenye stendi yake na kuiweka dirishani kwa mtindo uleule.

“Wanakuja!” akasikia sauti kutoka kwenye kifaa chae cha sikioni, sauti hiyo ya Amanda ilimpa taarifa.

“Ok!” akaitikia. Sekunde chache tu, akasikia king’ora cha gari la polisi huku nyuma yake kukifuata gari kama sita hivi zilizojipanga katika mtindo wa kupendeza.

“Gari ya tatu kushoto, ameketi katika kiti cha nyuma katikati!” Amanda akamwambia tena Martin.

Kijana huyo akapata kama ganzi hivi kwa kuwa alijua wazi kwa shabaha hapo patakuwa pagumu, hawakutegemea kwa kiongozi huyo kukaa katikati labda kama na wao wangekuwa chini.

“Hard Target!” akatamka.

“Tumia akili ya ziada!” Frederic akamwambia katika chombo kilekile. Martin alikuwa mzoefu sana katika kudungua, alijua kila aina ya shabaha katika kazi hiyo, kwa ujumla yeye alikuwa ni muuaji mwenye taaluma ya juu sana. Alijua wazi kuwa akikose shabaha tu basi atakuwa katika wakati mgumu kwani kanuni za mauaji ya namna hiyo ni hizo, risasi moja tu uwe umemaliza mchezo, hutakiwi kupiga risasi mbili kwa maana risasi mbili huzidi kufanya usalama wako kuwa matatani asilimia za kukamatwa au kugundulika zinapungua. Akiwa katika kuwaza hivyo, tayari ule msafara ulikuwa umekaribia umbali ambao shabaha yake ingeweza kufanya kazi.

Kutoka pale alipo, alifyatu usalama wa bunduki yake, na ile risasi ikingia chemba, kwa shabaha ya ajabu, akavuta trigger nyuma na kuiruhusu risasi ile iende ilikokusudiwa, hakujali kama imepata au imekosa, aliinuka haraka, akakunja miguu ya ile bunduki, kuifungua mtutu wake, akatia kwenye mkoba na kutoka haraka. Huku chini Frederick tayari alikuwa amewasha gari na hakupita muda, akamwona Martin akiingia garini naye akaondosha.

* * *

Ghafla, dereva wa gari la rais, aliyumba baada ya kusikia yowe moja tu la mheshimiwa. Magari mengine nayo haraka yakalizunguka lile la rais ambalo kidogo litoe nje ya barabara kama si umahiri wa dereva. Askari wenye silaha tayari walikuwa nje na bunduki zao. Dakika chache baadae helkopta ya serikali iliwasili ikiwa na madaktari, wakamchukua rais na kumpakia kisha wakaondoka eneo hilo kuwahi matibabu.

Jiji la Luanda lilikuwa kwenye hali mbaya siku hiyo, askari kaznu walimwagwa haraka kila kona na mshikemshike ulikuwa si wa kawaida.

Amanda aliwasili katika eneo la tukia kama dakika tano baadae na kukuta rais akiondolewa eneo lile huku askari wakiranda huku na kule. Akasimama mbali kidogo na ghafla akatakiwa kupita njia nyingine na si pale kwa kuwa tayari kuliwekwa utepe wa zuio.

“Nini kimetokea?” mkuu wa polisi wa jiji hilo aliwasili na kutaka kujua kutoka kwa vijana wake kilichotokea, lakini kabla hata hajapoke jibu akapigiwa simu na kutakiwa kufika Ikulu ya nchi hiyo haraka sana kwa kikao cha dharula.

Katika ukumbi wa mikutano ndani ya jingo la Ikulu ya nchi hiyo, viongozi wa juu wa maswala ya usalama walitangaziwa kuwa rais wan chi hiyo amefarika dunia kwa kupigwa risasi iliyomuumiza vibaya kichwani. Ilikuwa ni taarifa ya masikitiko si kwao tu bali kwa taifa zima.

Mara baada ya kuondoka pale, Fredric na Martin waliwasili Mbuga ya wanyama ya Kissama pembezoni kidogo mwa jiji hilo maana walijua mpaka dakika hiyo wasingeweza kutoka nje ya mpaka kwa njia yoyote ile.





ADDIS ABABA

TAARIFA ZA KIFO cha rais huyo zikafika Makao Makuu ya AU siku hiyohiyo na kuleta mtafaruku mkubwa miongoni mwa marais wan a wawakilishi mbalimbali waliofika kuwakilisha nchi zao katika mkutano mkuu. Rais wa Angol alikuwa ni mmoja wa wajumbe muhimu sana na mwenye hoja nzito ya kuwasilisha.

Nako kikao cha dharula kikakaliwa kuijadili hali hiyo, haikuingia akilini, swali kubwa lilikuwa ni; kwa nini na nani aliyemuua kiongozi. Vichwa viliuma akili ikasinyaa, hakukuwa na jibu, mkutano huo ukaahirishwa ili kwanza upishwe uchunguzi juu ya mauaji yale. Ilikuwa ngumu sana kujua kiini cha mauji hayo kwa sababu hakukuwa na taarifa ya madai wala uhasama. Kilichowekwa mezani na kujadiliwa ni ugaidi, kwamba ‘lilikuwa tukio la kigaidi’ basi hakukuwa na kingine. Baada ya wachunguzi waliobobea kwenye mambo ya kiuchunguzi kama haya walijiuliza sana ni vipi wataita ugadidi kama hakuna mkwaruzano wowote wa kisiasa kati ya nchi hiyo na magaidi, hawakupata picha ya moja kwa moja bali hata wao walibaki kuanza kutengeneza jibu kisha walifanyie kazi.



DAR ES SALAAM

Nchi zote za Afrika zilipata taarifa hiyo haraka sana ikiwamo Tanzania. Habari hii ilimkuta Madam S akiwa ametingwa afisini kwake, na ilipenyezwa kwake moja kwa moja kutoka Ikulu ya Magogoni. Akabaki amebutwaika pasi na kujua nini hasa kimetokea. Ni tatizo ililotokea nchi nyingine lakini yeye kama mwanausalama alitakiwa kufanya chochote katika hilo. Na yeye hakusita aliwataka vijana wake kufika katika ofisi ndogo na kuwapa taarifa hiyo ambayo wote waliipokea kwa mshangao na fikra tafauti. Lakii baada ya mazungumzo nao wakatakiwa kuhakikisha usalama kwa nchi yao.

“Nashindwa kuelewa huyo mdunguaji wanyemwacha anajinywea bia kwa raha zake wana mpango naye gani?” Amata akasema.

“Umeshaanza kuingilia kazi isiyokuhusu…” Madam S akamuonya.

“Ingekuwa hapa huyo hayawani asingepona, yaani mpaka sasa angekuwa anapumulia mipira…” akasema na jopo zima likacheka sana.

“Kwa hiyo sasa safari ya ya mheshimiwa Rais imeahirishwa, na haitakuwepo kwa sasa,” Madam S akawapa taarifa hiyo nao wakaafiki kabisa bila kuipinga.



MIEZI MINNE ILIYOPITA

ABIDJAN – IVORY COAST

WAKATI BADO Waafrika hawajasahau shambulizi lililotokea Angola, wakashitushwa tena na hili la Abidjan. Hili lilimlenga moja kwa moja Waziri Mkuu wa nchi hiyo. Siku alipokuwa akiandhimisha sikukuu ya Mtoto wa Afrika katika uwanja mkubwa wa michezo katika jiji hilo unaojulikana kama Stade Felix Houphouet. Siku hii ni siku kubwa sana Afrika ambayo husherehekewa karibu barani kote hukusanya watoto na viongozi mbalimbali wa serikali. Waziri Mkuu wa Ivory Coast alikuwa miongoni mwa watu ambao wangehudhuria sherehe hizo katika nchi yake.

“Tutamwondoa siku hiyo!” walipanga wakiwa mafichoni kwao katika mji wa Anyama ambako waliingia kama wiki tatu kabla ya tukio. Kama kawaida Amanda alitangulia kuiangia Abidjan kwa ajili ya kulichunguza windo lake na kujua ratiba na taratiu zte za maisha ya mtu huyo ili kujua ni wakati gani wa kutekeleza. Kilichofanyika ni kuwa wao walikuwa wakipewa picha tu kuwa ni nani anatakiwa aondolewe, hata sababu ya watu hao kuuawa hawakuijua, wao walitekeleza tu matakwa ya mteja wao, basi.

“Unafikiri hapo ni pazuri?” Martini akauliza.

“Kwa upande wangu, ndiyo, pazuri na panafaa sana, cha muhimu ni kujua tu ni vipi tutamaliza kazi na vipi tutaondoka.





“No! hapo si pazuri kwa upande wangu!” Martin akaeleza wasiwasi wake, “hujapata ratiba yake nyingine baada ya hapo?”

“Of coz baada ya hapo kuna tafrija fupi, imeandaliwa katika Hoteli ya Leopard, pembezoni mwa Bahari ya Atlantiki….”

“Baaassss hapo sasa mi nitamaliza kazi yangu kwa sekunde chache sana,” Martin akamkatisha Amanda, “tena ni muda mzuri sana, usiku, muda wa giza, unajua tofauti na kule Luanda ile nilipiga jiwe kichakani….”

“Lakini kwa shabaha ileile!” Frederick akamalizia.

Mipango yote ilisukwa ndani ya nyumba hii ndogo na kazi ikabaki tu utekelezaji, Amanda na Fred walienda zao mapema sana katika Jiji la Abidjan kwa ajili ya maandalizi ya shambulio wakimwacha Martin nyuma akiendelea kujifua tayari kwa kazi hiyo. Martin alikuwa muuaji ‘assassin’ aliyebobea katika kazi yake na aliijua vyema. Alipitia mafunzo ya ujasusi hasahasa katika edani hii ya kuetekeleza mauaji, hivyo alijua jinsi ya kuua kwa silaha, kwa mikono, kwa kutenegneza ajali au njia nyingine yoyote ile. Alipoachana na ofisi yake huko Ughaibuni akaamua kujificha kwa miaka mingi sana na hapa ndipo akaunda kikosi hiki maalum kwa kazi hii, kilichokodiwa na watu wenye mahitaji kama haya.

* * *

USIKU WA SIKUKUU YA MTOTO WA AFRIKA

KATIKA hoteli kubwa na ya kisasa yaani ya nyota tano ndani ya Jiji la Abidjan, iliyojulikana kama Leopard. Usiku wa siku hiyo, viongozi wa taasisi mbalimbali na mashirika yasiyo ya kiserikali walikusanyika kwa tafrija ndani ya ukumbi wa hoteli hiyo.

Saa tatu usiku, Waziri Mkuu wan chi hiyo Bwana Ayatou Al Assad aliwasili na wapambe wake huiku ulinzi ukiwa umewekwa nje ya hoteli hiyo na ndani pia. Baada ya kusalimiana na wale waliompokea nje ya jingo hilo, akaingia ndani kwa kusindikizwa. Yote haya Amanda alikuwa anayaona kutoka ndani ya gari lake alilokuwa akitumia ndani ya jiji hilo.

“Umeona?” akamwambia Martin

“Nimeona!” Martin akajibu.

“Mi nilikwambia, mchana ingekuwa muda muafaka sana kwa kazi hii,” akalalama mwanamke huyu.

“Sikia Amanda, najua nini unahofia, sasa kwa taarifa yako huu ni muda muafaka sana kwa mimi kumaiza kazi hii, utashangaa mwenyewe, tena nafikiri sihitaji kabisa hata silaha ya moto ni mikono yangu tu itakayoshughulika naye…” Martin akawaeleza wenzake.

“Sawa, sasa sisi tutakusubiri pale tulipokubaliana, sivyo?” Fred akamwambia swahiba wake naye akajibu kwa kutikisa kichwa.

Martin akashuka kwenye lile gari na kuwaacha wenzi wake wakiwa bado ndani yake.

“Kazi njema!” Amanda akamwambia huku Fred akimpa mkono. Wawili hao wakatia gari moto na kuondoka katika viwanja vya hoteli hiyo huku wakimwacha Martin akiwasindikiza kwa macho. Baada ya kuhakikisha kuwa lile gari limeondoka, Martin akachukua simu yake na kupachika vifaa vya kusikilizia, kisha taratibu akavuka barabara na kuelekea katika hoteli ile, akuufuata mlango mkubwa bali alifanya kama anapita njia na kuzunguka upande wa nyuma wa hoteli hiyo.

“Hey! Hey! Simama!” Martin akasikia sauti ikimwita nyuma yake, hakusimama akaendelea kutembea huku mikono yake ikiwa mifukoni, bado ile sauti ikazidi kumsimamisha, akasimama. Martin kutokana na ugeni wake hakujua kama upande anaokwenda kupita hauruhusiwi ndiyo maana alitakiwa kusimama.

“Njia imefungwa upande huo!” akaambiwa.

“Sasa tunapita wapi?” akauliza huku akiwa amejiandaa kwa lolote maana hakujau ni nini kitatokea kwa kusimamishwa huko.

“Oh samahani, sikujua kabisa juu ya hilo,” Martin akajibu na kugeuza njia kuufuata upande wa pili. Yule askari aliyekuwa anaongea akamwangalia kijana huyo akitembea kuelekea upande mwingine, akamtilia shaka. Akavuta hatua za haraka na kumnong’oneza mwenzake kisha wote wawili wakaanza kumfuata kwa nyuma kujua hasa ni wapi anakokwenda. Martin akajua hila zao, akaendelea kutembea kana kwamba hajui kama wanamfuata. Akafika kwenye kona na kukunja, kisha akajibana katika ya kuta mbili zilizoacha nafasi katikati, hakuonekana.

Wale askari wakafika kwenye ile kona nao wakakunja, hawakuona mtu, wakjikuta peke yao, si kwamba upande huo hakukuwa na mwanga, la, taa kubwa zilikuwa zikiangaza upande huo kwa usalama zaidi lakini askrai hao hawakuweza kumwona mtu huyo.

“Ghost!” mmoja akamwambia mwingine ambaye tayari alikuwa na bastola mkononi akirandaranda huku na huko.

“Kapotelea wapi huyu mtu?” yule wa pili akauliza lakini hakupewa jibu kwani hata wa kwanza alishazani kuwa huyo si binadamu bali ni mzuka tu. Kutoka kwenye pachipachi za kuta zile, Martin alikuwa akiwaona na kuwasikia kila walichokuwa wakizungumza. Utulivu na jinsi alivyojiranda na kuta zile isingekuwa rahisi kumgundua kwani hiyo ilikuwa ni moja ya mafunzo yake aliyopitia jinsi ya kujificha katika mazingira tofauti na kumpoteza adui yake. Kama dakika kumi hivi wale walinzi wakaondoka wakisikika kusema kuwa wankwenda kuchukua wengine zaidi kwani hata wao walionekana kwamba wana munkari ya kumtia mkononi. Walipotoka tu, Martin akajitokeza na kuwahi bomba kubwa la maji taka litokalo chooni, bomba hilo lilikuwa limeunganishwa kutoka vyoo vya ghorofa ya juu mpaka chini kabisa. Kwa kasi ya ajabu akakamata na kukwea kwenda juu kwa kutumia bomba hilo. Na alipofika kama ghorofa ya sita hivi akasikia huko chini sauti za watu wakizungumza, akatazama na kugundua kuwa ni wale askari sasa wamekuja wane zaidi jumla sita, akatulia na kujibana tena sambamba na bomba hilo. Hata wale askari walipoangaza macho yao juu hawakuweza kugundua kama kuna binadamu. Baada ya kujiridhisha kuwa hakuna mtu wakaondoka zao na kurudi kwenye malindo yao ya kawaida. Martin akaendelea mpaka ghorofa ya saba na kufika katika moja ya chumba ambacho kilimfurahisha, dirisha lilikuwa wazi. Kutoka katika bomba hilo mpaka kufikia dirisha hapakuwa mbali sana, alijivuta na kujifyatua mara moja mikono yake ikawahi kudaka kingo za chini za dirisha hilo, akatulia akining’inia kama sekunde arobaini hivi akaisikiliza kama kunamtu atakayekuja upande huo.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Zaidi ya sauti za mahaba zilizotoka ndani ya chumba hicho hakukuwa na mtu kuja dirishani wala nini, Martin akajivuta juu taratibu na kichwa chake kikavuka ukingo wa dirisha lile, naam juu ya kitanda kikubwa ni binadamu wawili ambao walikuwa juu yake wakipeana mambo ya kwenye video. Martin alijivuta na kuingia mzima mzima, akatua sakafuni taratibu, mita moja tu kutoka katika kitanda kile.

“Who are youuu!!!” yule mwanamke juu ya kitanda kile akapiga ukelele huku akimsukuma kwa nguvu mwanaume aliyekuwa naye akimchomoa mwilini mwake. Martin tayari alikwishachomoa bastola yake lakini hii haikuwa ya mauaji, akafyatua mara kadhaa na vijishale vidogo vikawaingia wawili hao nao haikuwa pa hata dakika moja wakakumba na usingizi mzito.

Nimefika! Martin akajisemea ndani ya ubongo wake kisha akajiweka sawa, akachukua nguo za mwanaume huyo zilizokuwa kando tu, akazivaa juu ya zile za kwake, zikamkaa vyema, akavua begi lake la mgongoni na kuliweka kando, ndani yake katoa waya wa piano ‘piano wire’, waya hatari sana katika kuvunjia shingo. Akaueka katika mfuko wake na bastola yenye risasi akaiweka vyema kabisa katika koti lake la suti. Akajitazama kiooni na kujiweka nywele sawia, tayari kuingia ndani ya tafrija ile.

“Tunasubiri taarifa kutoka kwako!” sauti ta Amanda ikayafikia masikio ya Martin kupitia earphone zile.

“Wait! The patient dog will eat a big bone! I am in!!” akawajibu kupitia njia hiyo hiyo. Martin tayari alikuwa amebadilika mwonekano wake, akafungua mlango na kupita kwenye korido ndefu mpaka kwenye lifti, akaingia na kuamuru irudi tena mpaka chini, akateremka na kuingia katika ukumbi huo wa waalikwa alipoulizwa mlangoni, akaonesha kadi ndogo aliyoikuta katika shati lile akaruhusiwa kuingia.

Hakukuwa na watu wengi, isipokuwa wachache wenye heshima zao na wazito, akazungusha macho kwa haraka na kuona mchezo gani anastahili kuucheza ili amalize alilotumwa. Kabla hajakaa kitini akavuta hatua na kuingia kwenye ujia ambao wahudumu walikuwa wakitokea kama wanaleta vinywaji. Mara moja alimkariri sura mhudumu wa kike ambaye alikuwa akimhudumia mheshimiwa waziri. Ndani ya chumba kidogo msichana yule aliingia tayari kuchukua chano ya vinywaji na kuipeleka, Martin alijua wazi kuwa chano hiyo kwa vyovyote inaeenda meza kuu, akajifanya anapita kuendelea na safari lakini haikuwa nia yake, mara yule msichana alipotoka akamjia kwa nyuma taratibu sana kwa mwendo ambao hauna kelele. Akiwa mkononi ana kinywaji kilichoshahabiana kabisa na kile ndani ya chano. Akakibadili taratibu bila yeye kujua kisha akamwambia.

“Samahani, heti maliwato ni wapi?”

Yule mwanadada akashtuka na kugeuka nyuma akakutana macho na kijana huyo wa kizungu.

“Oh sorry, huku umekosea njia, ni upande ule wa pili korido kama hii utaona milango,” akamwelekeza na kumwacha apite. Martin alipita pasi na kujulikana kama amebadili kinywaji kile.

Hatua kadhaa zikamfikisha upande ule, akaingia kama alivyoelekezwa, naama kulikuwa na milango miwili. Mmoja uliandikwa V.I.P akaupita na kuingia unaofuatia ambao kwa ndani umegawanyika mara mbii aani kushoto wanawake na kuume wanaume, akasimama na kutafakari kidogo. Akaingia choo kimoja cha wanawake kwani ndicho hasa kimepakana na kile cha VIP, ndani ya choo hicho akajifungia. Akajaribu kuugonga ukuta huo, akagundua kuwa si ukuta kama ukuta bali ni mbao laini zilitenganisha. Martin akatafakari jinsi gani atatekeleza azma yake hiyo, akili yake ikamwambia ‘umecheza pata potea’ lakini hakukubaliana nayo. Juu ya darai kulikuwa na taa kubwa imefungwa kwa mtindo wa pekee.

“Yes!” akasema kwa sauti ndogo na kupanda juu ya sinki la choo cha kukaa na kuing’oa taa ile kwa urahisi nayo ikamwachia tundu kubwa la kutosha, akakwea kwa ustadi na kuingia ndaani ya dari kisha akaivuta taa ile taratibu na kuirudishia. Ndani ya dari ile kulikuwa na uwazi ambao mtu angeweza kutambaa, akafanya hivyo mpaka kwa uangalifu na kusubiri pale alipoona kuwa patakuwa ni choo cha VIP. Akatazama saa yake ikamwambi kuwa ni saa tano za usiku.

Vipi kama asipokuja chooni? Akajiuliza.

Atakuja tu! Akajijibu.

* * *

Tafrija iliendelea, katika meza ambayo Waziri Mkuu aikuwako pamoja na viongozi wengine, yule mwanadada akashusha chano ya vinywaji na kumsogezea karibu chupa ile ya kinywaji akipendacho mheshimiwa yule. Kinywaji kikafunguliwa na mheshimiwa akamiminiwa, naye bila hiyana akapiga kama mafunda kadhaa hivi na kushusha bilauri tupu, akamiminiwa tena kiasi na ye akashukuru. Vikundi vya nyimbo vilikuwa vikitumbuiza na watu wakipata vinywaji kwa vitafunwa wakati Martini akiwa ndani ya dari ndogo kumsubiri mtu huyo.

Dakika kama tatu baadae, mheshimiwa akanyanyuka. Mlinzi wake aliyekuwa jirani akasogea na kuvuat kiti.

“Toilettes pour le moment,” (maliwato tafadhali,) akamwambia kisha akaongozwa. Hakuana aliyekuwa anajua kilichotokea, baada ya Martin kubadilisha ile chupa ya kinywaji aliweka nyingine ambayo imechanganywa na kiasi cha dawa aina ya Lasics ambayo ukiitumia utajisikia kukojoa mara nyingi sana.

Nje ya mlango wa choo cha VIP, yule mlinzi alisimama kuweka ulinzi huku mkuu akiwa kaingia ndani kumaliza haja zake, hakujua kama juu ya paa hilo kuna kiumbe ambacho kinasubiri kuichukua roho yake. Tayari Martin alikuwa keishaifyatua ile taa kwa ndani na kuiweka tenge makusudi na alipojiridhisha kuwa aliyeingia ndiye hasa amtakaye akauweka tayari ule waya kwa kuuzungushia mkono huu na huu kisha akauweka mrefu wa kutosha ambao angeweza kucheza nao.

Wakati mzee huyo yupo katikati ya haja ambapo hawezi kufanya lolote ndipo Martin akasukuma ile taa ikaning’inia upande mmoja, mheshimiwa akahisi na kuinua shingo juu kutazama, kabla hata hajasema au kupiga kelele tayari ule waya ulimnasa shingo na kuzunguka. Martini akavuta juu kwa nguvu na sekunde hiyo akavunja shingo na kuijeruhi vibaya, akaufungua upande mmoja na kuuvuta taratibu huku mwii wa kiongozi yule ukitua sakafuni tayaribu.

“Kazi imekwisha!” akanong’ona.

* * *

Nje, mlangoni, yule mlinzi akaitazama saa yake na ni muda huohuo Martin alimpita pale mbele yake akiondoka na asimtilie shaka. Dakika saba zikakatika, mlinzi akaanza kupata wasiwasi, akasubiri tena nyingine tatu zikawa kumi.

Siyo rahisi! Akaingia na kugonga mlango ndani, kimya, akagonga tena, kimya, kengele za hatari zikalia kichwani. Akaamua kuvunja mlango kwa kuwa aliruhusiwa kufanya hivyo kadiri ya mafunzo yao ya siri. Mara baada ya kufanya hivyo, macho yake yakagngana na mwili wa kiongozi huyo ukiwa chini ulimi nje.

Akatoa taarifa haraka na sekunde chache tayari palizingirwa na wana usalama, wakaanza kusaka huku na kule kujua ni vipi mtu huyo ameuawa, mshikemshike.

Taarifa zikaanza kufika kwa wanausalama, ‘kuna mtu waajabu tulimwona, shetani’ wengine nao wakasema yao. Pekuapekua, wakakuta zile nguo juu ya dari, wakazichukua kama ushahidi, nani mwenye nguo hizi kamera za usalama hazikuwahi kuficha kitu, zikamwonesha mtu mmoja mkubwa tu, Mkurugenzi wa shirika moja lisilo la kiserikali katika nchi ya Ivory Coast, kwa nini ameua? Utata. Lakini walipomsaka wakagundua yupo chumba nama 660 na kimwana wote wakakutwa wamelala usingizi mzito wakiwa kama walivyo, utata mwingine.

Usiku huu tafrija iliharibika, shughuli ikavurugika, hoteli ilifungwa kwa muda huku kukiwekwa katazo la mtu yeyote kutoka nje wala kuingia ndani ya hoteli hiyo. Askari wenye mbwa wakawasili tayari kusaka nyayo za muuaji.

* * *

Martin Gupter mara baada ya kuhakikisha keshamvunja shingo mtu wake, akatambaa mpaka pale alipoingilia, yaani choo cha wanawake, akashuka na kuvua zile nguo kisha akazitupia darini nay eye kutoka na nguo zake za mwanzoni. Alipita nje ya mlango wa choo cha VIP na kumsalimu yule mlinzi kwa ishara ya mkono. Moja kwa moja akapanda lifti mpaka ghorofa ya sita na kuingia katika kile chumba, akawakuta watu wake bado hawajaamka. Alichokifanya ni kuchukua begi lake na kuchomoa vile vishale kwa wale jamaa kisha akateremka chini kwa kutumia ngazi za dharula na kupotea huku akiacha kizaazaa hotelini hapo.

‘Kuh! Kuh! kuh! Kuh!’ dirisha la gari walimokuwa Amanda na Fredy likagongwa. Fred akafyatua loki na kijana huyo akajitoma kwenye siti ya nyuma.

“We go!” akawaambia na Fredy akaingiza gari barabarani na kuondoka kwa kasi.

“Umemaliza?” Amanda akamuuliza huku akigeuka nyuma.

“Bila shaka, kwa dakika hii taifa halina Waziri Mkuu, Afrika itaomboleza,” Martin akajibu kijeuri huku akibadilisha shati lake ndani ya gari hilo, “breki wapi wapendwa?”

“Anyama!” Fredy akajibu.

“Mbona mbali sana, mnajua inabidi tupite mahali tupoze koo huku tukitazama luninga kujua nini hasa kinaendelea huko mjini,” akawashauri nao wakazingatia gari ikaiacha barabara kuu ya Autoroute du N na kuingia ile ya Francois Mitterrand mpaka kwenye hoteli nyingine ya kawaida tu na kuweka gari lao hapo.

“No twende kupaki gari mbele kisha turudi kwa mguu,” Amanda akawaambia, wakakubali na kuendelea mbele mita kama mia mbili hivi, wakaliacha kati ya magari mengine kisha wenyewe wakarudi na kuketi ndani ya baa kubwa ya hoteli hiyo kandoni tu mwa barabara.

Kama ambavyo walifikiri ndivyo ilivyokuwa, macho na masikio ya watu wengi katika baa hiyo yalikuwa katika habari ya dharula usiku huo nayo ilikuwa inahusu kuuawa kwa Waziri Mkuu.

“Tayari!” Martin akasema huku akigugumia pombe kali aliyokuwa akiletewa.

“…mauaji hayo yametokea usiku huu katika hoteli ya Leopard. Vyombo vya usalama vinamsaka mtu anayesadikiwa kuwa ndiye aliyetekeleza mauaji hayo ambaye mpaka sasa hajulikani alipo lakini duru hizo zimemuhofia mtu asiyejulikana ambaye alionekana kuficha sura yake mara akutanapo na kamera za usalama….”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Hakuna mtu wa kunikamata kijinga hivyo najua kucheza na kamera najua kucheza na watu wa usalam, mimi mwenyewe nimeshakuwa huko kwa muda mrefu…” Martin akajigamba. Dakika arobaini na tano baadae wakaondoka zao na kuelekea Anyama katika nyumba waliyoelekezwa kuishi pindi wawapo katika nchi hiyo.





Ndani ya DIAMOND JET

JAFFER BAKHARI akazima luninga na kushusha pumzi ndefu akiwa ndani ya ndege ya kukodi ya kisasa aina ya Diamond Jet. Safari ilikuwa ni kutoka Uingereza kuelekea Somalia kwa minajiri ya kukutana na watu wake wachache katika Jiji la Mogadishu tayari kuanza rasmi kazi waliyopanga. Pembeni na yeye katika kiti cha mbele yake na kushoto kwake kulikuwa na watu wawili waliofanana naye kimuonekano.

“Afrika inaomboleza!” akasema kwa lugha ya Kibakhrein, wale jamaa wawili wakawa kama wamegutuka na kumtazama.

“Vipi?” mmoja akauliza.

“Tayari, Waziri Mkuu wa Ivory Coast amekwenda na maji…”

“Aaaaaah nilikwambia comrade! Kile kikosi sikukosea kukikodi, umeona kazi inakwenda kwa muda tuliopanga, sasa tukifika tu tuwape ujumbe kuwa ni sisi na nini tunataka, AU lazima ikubali matakwa yetu,” yule mjumbe wa mbele yake akamwambia kwa furaha.

“Hah! Hah! Hah! Hah! Nauona ushindi! Cheers….” Akafurahi na kugonga nao bilauli zilizojaa kinywaji kitamu, “Chukua camera, nitaka niwape ujumbe watu hawa kisha uwatumia mara moja waupate…” akawaambia na mmoja wao akafungua begi dogo na kuchukua kamera ya picha mjongeo akaitega tayari. Jaffer Bakhari akavaa kitu kama soksi nyeupe na kuificha sura yake kisha akaanza kuzungumza.



“Tulituma barua nzuri sana kwenu, tukawaaambia kuwa tunahitaji nusu ya nchi ya Somalia iwe huru na ijitawale kwa kuwa Serikali yenu ambayo ni mwanachama wa AU mmeshindwa kuwasaidia watu hawa.

Kwa ujeuri wenu mkapeleka majeshi yenu na kuwapiga vibaya watoto wetu waliokuwa wakiitetea ardhi yao, wakitaka kuikomboa nchi ya mama zao. Haya ni maonyo, mauaji ya Angola Luanda ni sisi tumeyatekeleza kwa kuwa marehemu yule alikuwa mstari wa mbele kupinga hoja ya Somali land kugawanywa. Saa kumi na tano zilizopita tumemuondoa Waziri Mkuu wa Ivori Cost kwa kuwa naye ndiye aliyeiondoa shilingi mezani na kulifisha ombi letu.

Tuliwaambia damu ya watoto wetu haitaenda bure, nchi yetu ya ahadi lazima tuipate iwe kwa damu au kwa maji…

Tunaomba nchi yetu, tunaomba haraka kabla hatujamwangusha mwingine…”



* * *

ADDIS ABABA

KATIKA OFISI NYETI ya makao makuu ya Umoja wa Nchi za Afrika video yenye ujumbe ule ilifika kwa anwani pepe ya umoja huo. Alikuwa katibu muhtasi wa Mwenyekiti wa umoja huo aliyeupokea. Alipoutazama, akapiga na butwaa lisilokifani, hakuchelewa, alimwita mhusika ambaye humuwakilisha mwenyekiti huyo afisini kama hayupo akamwonesha.

“Shiiiiittt!!!” akaunguruma na kuchukua simu akapiga kwa bosi wake. Mwenyekiti wa Umoja wa Nchi za Afrika Rais wa nchi ndogo ya Gambia akaupoke ujumbe huo hukohuko aliko. Hatua ya haraka aliyoichukua ni kuitisha kikao cha wajumbe watatu wa juu wa umoja huo akiwamo mkuu wa baraza la Usalama pamoja na yeye kukutana mara moja na haraka katika ofisi hizo.

Mchana wa siku hiyo wote wanne walifika kwa nyakati zilizopishana kidogo, hakuna aliyetafuta hoteli ya kukaa badala yake wakafikia katika chumba cha mikutano.

“Nadhani nyote mmesikia yaliyotukia Ivori Coast jana usiku!” Akawaambia, nao wakatikisa vichwa, “tunawindwa, baada ya kifo cha Rais wa Angola ambacho upelelezi mpaka sasa unaendelea jana tumepoteza kiongozi mwingine mkubwa tu Afrika. Muuaji au wauaji wamejitokeza na huu ndiyo ujumbe wao kwetu…”

Akawawekea ile video kwenye luninga kubwa ndani ya chumba kile, na wote wakatazama na kuirudisha kama mara nne hivi kana kwamba walikuwa wanataka kukariri kinachozungumzwa. Baada ya kuizima kila mmoja akashusha pumzi ndefu.

“Ina maana huyu ndiye anayeendesha vuguvugu lote kule Somalia?” Mjumbe mmoja akauliza kwa hasira.

“Si umemsikia, ni yeye, ameahidi kutekeleza hiki anachofanya mpaka tukubali matakwa yake na watu wake!” Yule mwenyekiti akawaambia wajumbe.

“Huyu mtu ni kichaa? Anataka tuigawanye nchi ili yeye na wajinga wenzake wafaidi mafuta? Haiwezekani, nitapinga kwa nguvu zote…!” Mwenyekiti wa Baraza la Usalama akang’aka, lazima akamatwe ili ajue kuwa hatuchezi na vichaa kama yeye” akasema.

“Hatutakiwi kumfumbia macho, lazima tumfanyie kazi…” Mwenyekiti ambaye ni rais wa Gambia aliongea kwa sauti ya chini na wajumbe wake wakatikisa vichwa juu chini. Akatoa maagizo ya kazi kwa wajumbe wale nini ya kufanya dhidi ya hali hiyo huku akituma ujumbe kwa marais wote wa Afrika wajue ni nini kinaendelea. AU ikatuma wapelelezi huko Somalia kwenda kufanya uchunguzi ikiwezekana kubaini kama watu hawa wapo huko au la.







MTO LOFA – SIERRA LEONE

Rejea sasa…

WAVUVI walikuwa wakiendelea na shughuli zao za uvuaji samaki kama kawaida katika mto huo mkubwa unaomwaga maji katika Bahari ya Atlantiki. Boti kubwa ilikuwa ikikata maji kuelekea upande wa bahari hiyo kuendelea na shughuli hizo, mbele kidogo wakapunguza mwendo na kupiga nanga kisha wakashusha nyavu kuvua samaki kama kawaida. Mvua kubwa yenye radi kali ilikuwa ikipiga kwa hasira, wavuvi hawa, kama sita hivi walikuwa wamejifungia ndani wakisubiri mvua hiyo yenye upepo wa mbisho ikome lakini haikuwa hivyo.

“Hey, naenda kwa sigareti kidogo!” jamaa mmoja aliyejulikana kwa jina la Hamadou akawaaga wenzake na kuinuka kilagoni, akatwaa koti kubwa refu la plastiki, sigara akaipachika kinywani na kuibana na midomo yake miwili, akatoka nje. Bado mvua kubwa ilikuwa ikipiga huku radi zikifuata. Akiwa anavuta sigara yake, macho yake yakaona kitu kama binadamu anayetapatapa kwa kuchoka ndani ya maji.

“Shiiiiiit! Hasssan! Hasssan!” akaita kwa nguvu na mara wenzake wakatoka haraka kumfuata kuel nje.

“Hamadou, nini tena?” mmoja akauliza.

“Yule mtu anakufa, yuleee, tumsaidieni jamani…” akiwa katika kusema hayo, tayari Hassani alikwishavaa boya kubwa na kujifunga kamba ndefu kiunoni, akajitoma majini huku wenzi wake wakiishika ile kamba kusudi maji hayo yasimsombe. Hekaheka huku na huku, kama dakika arobaini na tano hivi walifanikiwa kumwingiza ndani ya boti lao mtu huyo.

“Bado mzima?” Hamadou akauliza.

“Bado ila mwili wake inaonekana ana baridi sana, inabidi tumuweke kwenye joto…” Hassan akatoa ushauri nao wakafanya hivyo. Wakamteremsha chumba chini ambako hutumia kwa kupika, wakamlaza juu ua bao kifudifudi na kumpa huduma ya kwanza huku wakiwa tayari wamewasha moto.

Hassan na wengine wakatoka nje na kumwacha Hamadou akiendelea kumfanyia huduma ya kwanza ili angalau mtu huyo apate nguvu. Mungu mkubwa, baada ya kama saa moja hivi, akaanza kurejewa na nguvu kidogo, akaanza kufumbua macho na hata kutikisa mkono kidogo. Hassan akawaita swahiba zake ambao walikuwa bize wakiendelea na uvuvi baada ya mvua ile kunyamaza.

“Vipi? Anaendeleaje?”

“Ameamka sasa nataka nimpatie uji,” Hamadou akajibu huku akichukua bakuli lenye uji wa kienyeji. Wakamkalishsa vizuri, wawili wakamshikilia huku na huku na Hamadou akaanza kumnywesha uji ule kijiko kwa kijiko. Baada ya bakuli lile kwisha, wakamwacha apumzike chini kisha wao wote wakaenda kuendelea kufanya kazi. Saa moja baadae wakapiga nanga katika mji mdogo wa Waterloo. Hassan alipoingia tena kule chini alipomwacha mgonjwa wake hakumkuta. Akaangaza macho huku na kule na kugundua kuwa mlango wa kutokea nje upande wa nyuma upo wazi, akauendea na kuusukuma akamkuta mtu huyo amesimama nje akitazama mandhari ya mji huo mdogo.

“Hey man! Are you ok?” akamuuliza kwa kiingereza cha kubabaisha. Hakuitikia badala yake akarudi ndani na kufuatan na mwenyeji wake mpaka nje ya boti hilo. Wakati wengine wakiendelea kupakua samaki kwa wauzaji wao, Hamadou alitoka na mtu yule na kumpeleka katika nyumba ndogo, mwendo mfupi tu kutoka katika bandari hiyo.

Ndani ya nyumba hii kulikuwa na mwanamke mmoja mtu mzima kiasi, kama miaka mitano mkubwa zaidi yake.

“Huyu ni rafiki yangu, naomba umpatie tiba ana kidonda kichwani kisha nitakuja baadae kumchukua!” Hamadou akamwambia yule mwanamama kwa kifaransa kisha akampatia pesa kidogo na kuondoka, yule mwanamama akamjia mgeni huyu na kumtaka alale kifudifudi, akawasha moto na kuchemsha dawa zake za kienyeji na kumpa tiba ambayo jamaa huyu hakuwahi kuiona maishani mwake. Baada ya pumziko kama la saa mbili hivi akajisikia ana nguvu na maumivu yote ya mwili yametoweka.

Niko wapi? Akajiuliza, hakukuwa na wa kumjibu, akainuka kutoka pale kitandani na kusimama wima sakafuni. Nyumba hii ilikuwa ndogo ya wastani, haikuwa na vitu vingi ndani zaidi ya kitanda na chupachupa nyingi sana zilizopangwa katika shelfu kuukuu. Ukutani kuikuwa na mapichapicha mengi tu yaliyofubaa kwa moshi. Alipojipapasa kisogoni hakuhisi maumivu isipokuwa tabaka kubwa la kitu kama udongo au sijui tuiteje. Yule mwanamke alikuwa amembadika lundo la majani yaliyotwangwa na kuchemshwa na kuchanganywa na miti shamba ya kutosha.

Dawa! Akawaza.

Mwili wake ulikuwa na nguvu mpya kabisa, hakuamini, akatembea kidogo na kujikuta yuko fiti.

“Unajisikiaje?” akasikia sauti ikimuuliza kutoka nyuma yake, akageuka na kumwona yule mwanamama akiwa kasimama mlangoni. Mgonjwa huyu hakujibu kwa maneno, akatikisa kichwa juu chini na kuonesha ishara ya dole gumba kuwa yuko sawa kabisa. Mwanamama yule akatoa tabasamu pana lilioacha vishimo mwororo mashavuni mwake.

* * *

DAR ES SALAAM

Gina akaweka mezani bahasha ya kaki, kisha akaisukuma nayo ikaserereka mpaka kwa Chiba aliyeketi upande ule.

“Hiyo hapo!” akamwambia.

“Imekamilika?”

“Bila shaka!” akamjibu kisha akajiinamia kimya.

“Vipi unawaza nini shem…” Chiba akamtania.

“Unanitia uchungu Chiba, nenda haraka tafadhali, natamani kama ningetumwa mimi vile,” Gina akamwambia Chiba kisha akanyanyuka na kupotelea katika vyumba vya ndani ya jengo hilo. Chiba akabaki peke yake katika meza hiyo, akaifungua bahasha ile na kuichungulia ndani, pasipoti, tiketi na pesa kidogo na kadi moja ya benki yenye uwezo wa kutoa pesa mahali popote duniani.

“Uko wapi Amata?” akajisemea kwa sauti.

“Ukiukosa mwili wake liletee taifa medali ya shujaa wao!” Gina akasema kutoka upande wa pili. Wakiwa bado katika hali hiyo, mngurumo wa gari ukaanza kusikika kwa mbali katika vyombo maalumu ambavyo Chiba amevitenga kwenye jumba hili, vyenye uwezo wa kunasa muungurumo wagari umbali wa kilomita moj na kuupembua kujua kuwa kama ni gari yao au la.

“Bibi anakuja!” akamwambia Gina kisha akawahi kukaa katika luninga zake na kutazamakujiridhisha kama ni kweli au la. Dakika hiyohiyo simu ikaita, akainyakuwa na kuiweka sikioni…

“Yes!” akaitikia.

“Kuna mzigo umeingia hapa nina wasiwasi nao!” sauti ya upande wa pili ikamwambia.

“Nipe picha!” Chiba akamwambia mtu huyo kisha akatega jicho kwenye luninga yake.

“Nani huyo?” Gina akauliza.

“Lulu…” akajibiwa.

Sekunde chache tu, kwenye luninga ile ikafika picha ya mwanaume mweusi, pande la mtu, anayeonekana kushupaa mwili kwa mazoezi. Nywele zake ndefu zilisimama kwa mtindo wa Afro, miwani myeusi iliyaficha macho yake na kumfanya asionekane sawasawa. Chiba akaingia kwenye mtandao wa utambuzi, akaingiaza sura ile na kuichambua, mamilioni ya sura, alama za vidole na majina vikapita kwa kukimbia kwenye kioo hicho na baadae vikasimama.

“George Sabatth!” akatamka, “kutoka Msumbiji,” Chiba akamwambia Gina huku akiendeela kusma taarifa za mtu huyo.

“Ni askari?” Gina akauliza.

“Inaonekana hivyo, tazama!” akamwonesha maelezo ya ziada ya mtu huyo, yanayoonesha wasifu wake kuwa ni askari mwanajeshi, aliyepitia mafunzo mbalimbali ya kijeshi na kushiriki operesheni nyingi za ndani na nje ya nchi yake. Aliacha kulitumikia jeshi la Msumbiji na kuanza shughuli zake za biashara ambazo anaendelea nazo. Maelezo haya Chiba akayaelewa vyema, akayaprinti kwenye kifaa chake na kuyaweka kando.

Punde tu, Madam S akaingia ndani ya jingo hilo na kujitupa kochini akiwa amechoka.

“Vipi Madam!?” achiba akamuuliza.

“Mission aborted!” akamjibu.

“Kivipi mama?” Chiba akauliza kwa shauku.

“Imeamuriwa kuwa, kutoka Tanzania tusitishe operesheni kwa sababu tumekuwa kimya siku tano wakati makubliano yalikuwa ni siku tatu kupeleka ripti ya wapi tumefikia…” Madam S akawaambia Chiba na Gina. Wawili hawa wakatazamana, kisha wakamtazama Madam S.

“Kwa hiyo!”

“Nenda ukamtafute kaka yako, uniletee jibu haraka iwezekanavyo mi washantia hasira…. Kimeundwa kikosi kingine kwa ajili ya kazi hiyo, kitajumuisha wapelelezi kutoka Maghalibi, Kaskazini na Kusini, kanda ya Mashariki imeondolewa kabisa,” Madam kaeleza wazi bila kuficha.

“Anhaaa, nahisi huyu aliyeingia ni mmojawapo… Madam… kuna kitu ninachoanza kukihisi, mi najaribu kuhisi kitu mama, hawa ndiyo walioshabikia Tanzania iingie kazini, si ndiyo hawa hawa, sasa leo nini kinawasibu wasitishe zoezi? Wana maslahi au?” Chiba akazungumza, “wacha nikamtafute kaka yangu, kwanza najua atawasiliana na sisi muda si mrefu,” akatania.

Wakiwa katika kuzungumza mara simu ikaita, hii ni ile ya Madam S ambayo huita kwa nadra sana, akaitazama, ‘private call’. Akampa ishara Chiba akafyatue kifaa chake tayari kurekodi ujumbe huo.

“HOT! HOT! HOT!” sauti ya upande wa pili ikaita.

“Roger! Roger!” Madam akaitika kisha akaongeza neno la siri ambalo huwatambulisha watu hao kama idara, “State of living…”

“Living of state!” akajibiwa kutoka upande wa pili.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Madam S na Chiba wakapasuka kwa furaha baada ya kusikia na kuihakikisha sauti hiyo, “Hakikisha kama ni yeye, Chiba!” Madam akasema huku akiwa amefunika sehemu ya kunasa sauti. Chiba akawasha mtambo mwingine ambao ambao huoanisha mawimbi ya sauti na huweza kukutambua muongeaji ni yeye au kaiga sauti kutokana na mkandamizo wa mawimbi hayo. Wakati Madam anaonngea na mtu huyo yeye alikuwa akifanya hilo zoezi kwenye chombo hicho huku akimwonesha alama ya ‘dole’ Madam S kumhakikishia kuwa aongeaye ndiye yeye.

“Upo wapi Amata?” akauliza.

“Madam, bado sijajua nilipo lakini naweza kusema kuwa nilikuwa nimekufa kabisa, na sasa nimefufuka,”

“Oh! Come on! Pole sana, tumekutafuta sana Kamanda, mpaka hapa tunapoonge mission imefungwa kwa kwaupande wetu, wanaunda kikosi kingihne kuendelea na kazi hiyo,” Madam akamwambia kijana wake.

“Waache wafunge, ila hawa jamaa siwaachi, mambo walionifanyia, lazima niwafungie kazi,” Amata akasema kutoka upande wa pili.

“Najua! Sasa Chiba anaondoka hapa usiku huu, safari yake ni Liberia kukutafuta, cha kufanya sasa ngoja tuone uelekeo wa simu ili tubadili safari, ila usitoke ulipo mpaka afike,” akamsisitiza.

“Sawa Madam! Tafuteni kupitia simu hii, ndiyo ya mwenyeji wangu…”

“Mwenyeji wako!”

“Yes, ni stori ndefu utaijua baadae!” akamwambia kasha akakata simu. Madam S, akaitusimu yake na kumnwendea Chiba.

“Vipi?”

“Nimempata… yupo Sierraleone jirani sana na Freetown, nafikir cha msingi ni mimi kufika Freetown si Monrovia tena, kasha kutoka pale nitajua jinsi ya kumpata,” akamwambia Madam.

“Safi, nilikwambia TSA1 huwa hafi kizembe,” baada ya kusema hayo Madam S akamwita Gina na kumpa maagizo mapya ya kutafuta ndege kufika Freetown. Kasha akaendelea na Chiba.

“Hakikisha unabeba GPS chip, nahisi wamemng’oa na kuiharibu ndo maana tulishindwa kujua alipo,” akamwambia.

“Aaaaa asante Mungu, nilikuwa nimejawa na hofu sana…”

“Kwa nini?”

“Nilikuwa nawaza ni jinsi gani viatu vya TSA 1 vitanitosha au kunipwaya!” akasema.

“Aaaaaannnhhh pole sana!! Sasa nina amani naweza kunywa whisk ikapita shingoni,” Madam akawaambia kisha akaondoka na kuwaacha Gina na Chiba wakiendelea na mipango mingine.

* * *

SIERRA LEONE

“Lugha ghani umekuwa ukiongea?” Yule mwanamama akamwuliza Amata.

“Kibemba!” akamjibu.

“Kibemba? Kutoka nchi gani?” akazidi kuchimba.

“Aaaaa huko kusini mwa Zambia,” akamjibu.

“Sasa ilikuwaje mpaka ukazama mtoni? Mto huu una mamba sana, mshukuru Mungu wako!” Yule mwanamama akamwambia Amata huku akiendelea kuchochea kuni ili moto uwape joto dhidi ya baridi kali eneo hilo. Kamanda Amata alitulia kimya, na ni dakika hiyo akagundua kuwa amevaa mkanda wa ziada kiunoni.

“Nini hiki?” akajiuliza. Akaushika ule mkanda na kuufungua, akautoa, kumbukumbu yake ikamjia akakumbuka mateso ya ndani ya lile kabiri, akamkumbuka yule mtu aliyempatia huo mkanda. Zaidi akakumbuka kwa Yule mtu alipata vitu vingine binafsi, kijitabu kidogo, akajipapasa na kukikkuta, akakitoa na kukishika mkononi, kimelowa japo unaweza kusoma maandishi kadhaa, akakumbuka ile karatasi, akaichukua kutoka mfukoni mwake, haikuwa ya kawaida ni kipande cha noti ya Euro 100.

“Mh!” akaguna kasha akaviweka karibu na moto japo view vikavu zaidi ya pale.

“Mbona umechana hela?” Yule mama akauliza.

“Sijachana, imechanika, na ndiyo pesa pekee niliyonayo,” Amata akajibu.

“Pole sana! Sisi huku hatumiliki pesa, kwani hta ukiwa nayo waasi huja kutupora na kutufanyia mambo ya ajabu ajabu,” akaeleza.

“Mumeo yuko wapi?”

“Ameuawa! Ameuawa na waasi kwa kuwa walitaka pesa yake ya biashara akawanyima!” akajibu.

“Pole sana!” Amata akamfariji na mara hiyop akamwona mwanamama Yule akiangusha machozi, akasogelea na kumkumbatia kwa nguvu.

“Hamadou ni nani?” akamuuliza.

“Ni kaka yangu…”

“Ok!”

Baada kama ya dakika tano za kumkumbatia akamwacha huru.

“Nimefarijika sana…”

“Kwa nini?”

“Sijawahi kukumbatiwa na mwanaume miaka mine sasa!” akamwambia huku akitabasamu, vishimo vya mashavu yake vikaonekana dhahiri shahiri. Amata alijikuta akitaka kuingia kishawishini, akajizuia na kuinuka pale alipoketi na kutoka nje.

Akiwa peke yake, akachukua tena kile kjitabu kidogo ambacho ndani yake kilikuwa kimeandikwa mambo mengi sana lakini kwa lugha tofauti tofauti. Ilikuwa ngumu kuelewa ni nini hasa kimeandikwa ndani yake alijaribu kupekuwa kurasa hii na ile, lakini bado hakuweza kuelewa yaliyoandikwa ilikuwa ni lugha iliyotumia alama zaidi.

Huyu ni nani? Akajiuliza huku akikitazama kijitabu kile, akakitia mfukoni na kuichukua ile noti na kuitazama kwa makini sana.

“Kwa nini wameichana?” akajiuliza kwa sauti ya kunong’ona, hakuna wa kujibu.

* * *

MWAKA MMOJA NYUMA…

Four Season Hotel – Bahrain Bay

Ndani ya hoteli hii kubwa na ya kisasa, iliyojawa kila wingi wa fahari ya dunia, mkutano mfupi ulikuwa ukiendelea. Mkutano huu ulihusisha watu sita, watatu Wazungu na wengine Waarabu wenye pesa.

Jaffer Bakhari na wafuasi wake watiifu wawili walikutana usiku huu katika hoteli hii. Upande wa pili wa mkutano huo kulikuwa na Amanda Keller, Martin Gupter na Frederick.

“Tumepata taarifa ya kutuita hapa… tumefika!” Martin akazungumza.

“Naam!” swahiba wa Jaffer akaitika… “nashukuru kwa kuwa mmeitikia wito, bwana wetu ana neno la kuwaambia.

“Nimeambiwa kuwa ninyi ni watenda kazi wazuri sana kwenye swala zima la assassination, sivyo?” Jaffer akawauliza.

“Naam, ni sisi …”

“Ok, tuzungumze biashara itakayodumu kwa miaka miwili…” Jaffer akawaambia.

“Weka pesa mezani kabla hujatuambia juu ya biashara hiyo,” Martin akasema.

Jaffer akanyosha mkono wake na yule swahiba wake akainua briefcase na kuiweka mezani, ikafunguliwa na noti za kutosha zikaututumua mfuniko wake. Martin akatikisa kichwa na kuisukuma kwa Fred naye akafanya vivyo hivyo mpaka kwa Amanda.

“Lete kazi!” Martin akasema.

“Good! Maelekezo ya kazi mtayapata ndani ya brieface hiyohiyo, kisha tutawasiliana kwa siri kila inapobidi, kwa kifupi nataka muitetemeshe Afrika,” Jaffer akamaliza na kusimama, akapeana mikono na wote watatu kisha akatoka ndani ya chumba kile na wale vijana nao wakaondoka.

* * *

HOTELI RIVERFRONT – Bahrain

VIJANA WALE WATATU wakaingia ndani ya hoteli hii ambapo Martin alikuwa amepanga chumba kwa siku hizo ambazo walikuwa katika nchi hiyo. Ndani ya chumba hicho akaitupa ile briefacase kitandani na Amanda akaiweka sawa na kuifungua kwa namba walizoelekezwa. Kutokana na pesa nyingi ambazo zilishindiliwa ndani yake lilifunguka kwa shida.

“Yeeeeeeeaaaaaaaaahhhhhhhhh!” akpiga kelele huku akizichota zile pesa na kuzimwaga ovyo. Akiwa katika kufanya hivyo akajikuta amaechukua bahasha kubwa nyeupe ndani yake.

“What!” akashangaa. Akaichukua na kuichana, ndani yake kulikuwa na karatasi ndogo ya ukubwa wa A5 pia kulikuwa na picha nne za ukubwa huo huo. Martin yeye hakushobokea pesa, akazitwaa zile picha na ule ujumbe akaketi kwenye meza ya kando, konani mwa chumba kile.

Katika ujumbe ule kuliandikwa sentensi moja tu.

‘Ninahitaji wauawe kwa gharama yoyote ile kama ilivyopangwa nyuma ya kila picha’

Ujumbe ule ukaishi hapo, Martin akachukua zile picha na kuzitazama moja baada ya nyingine, kweli zilikuwa na muda maalumu wa kuuawa watu hao kwa kitambo cha miezi miwili miwili. Martin alitazama kwa makini picha hizo na kupigwa na mshtuko wa moyo, akawaita wenzake waliokuwa wakihesabu pesa na kuwapatia. Wa kwanza alikuwa Amanda, akatazama zile picha, akamtazama Martin.

“Martin! Fredy!” akaita kisha akatulia, “hii kazi ngumu kati ya zote ambazo nimewahi kuzifanya… huyu ni rais wa Angola, sura yake si ngumu kabisa kuitambua, huyu ni Waziri Mkuu wa Ivori Coast, huyu hapa mwenye ndevu nyingi ni Rais wa Gambia na huyu mwembamba ni Waziri wa Ulinzi wa Togo….” Amanda akasema.

“Shiiiiittttt! Unawajuaje? Huyu na huyu ndiyo wanajulikana na hawa wawili,…” Martin akashangaa, yeye kwake haikuwa kazi ya kumsumbua kichwa kuwamaliza watu kama hao kwa sababu tayari ameshapitia kazi za kiintelijensia na hasa za kulinda viongozi hivyo huwa si mgeni na itifaki kama hizo.

“Nawajua… ila dah! Tutachomoka kweli kwenye kazi hii swahiba?” Amanda akaonesha shaka.

“Dah nini, kazi si tumeikubali, ni kweli ni kazi ya hatari sana, lakini msiumize kichwa huwa najua protokali zote na nakuhakikishieni tutawini, hizi pesa ni utangulizi tu lakini kuna hii kadi hapa, tazama…” akawapa ‘Maestro Card’, “kadi hii tutatumia pesa popote tutakapo duniani, tutalala popote pale pa gharama yoyote ile… kwa hiyo hata kutoroka na kujificha kwetu haitakuwa tatizo sana, cha muhimu tu ni kufanya kazi ya tajiri,” Martin akawaambia wenzi wake waliobaki kimya, kisha akachukua kiberiti na kuziwasha zile picha, akaziteketeza kwa moto. Akawatazama wenzake,

“Sasa ipo hivi, Amanda kwa hii utakuwa saveya, umjua tunayemtaka, ukusanye taarifa zake, upate ratiba zake zote, kwa hiyo utatakiwa mara kwa mara kuzipenya ngome ngumu za mashirika ya kiusalama katika nchi hizi na watu wanaowazunguka viongozi hawa. Fredy, utakuwa kwenye hatua ya tatu, ya jinsi gani tutaondoka katika eneo la hatari siku hiyo, mimi nitafanya kazi ya kudungua au hata ikibadi basi nitaingia kwenye kombati ya mkono kwa mkono, azini nitahakikisha tunawaangusha kwa gharama yoyote”, akamaliza na kuinuka pale alipoketi.

“Sawa, nipe change mi nikaandae kazi nitawaambia, kumbukeni tuna miezi isiyozidi nane kumaliza kazi hii,” Amanda akasema.

“Siyo shida,” Martin akaliendea lile sanduku na kuchukua maburungutu kadhaa akampatia mwanamama huyo, naye akayapokea na kuyasunda kwenye mkoba wake. Vivyo hivyo aka chukua mengine na kumpa Fredy, kisha nay eye akachukua ya kumtosha, kwa ujumla walichukua pasu kwa pasu na kuacha mengine mengi kwa kuwasaidia baadae. Baada ya hapo kila mmoja akatawanyika na kusubiri nini Amanada atawaambia kwa kutekeleza mauaji hayo.





Rejea SASA…

Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa LUNGI

FREETOWN – SIERRA LEONE

CHIBA WA CHIBA aliwasili katika uwanja huo mkubwa kabisa usiku wa saa nne, mara tu baada ya kutoka nje hakutaka kupoteza muda kwani alikuwa na mengi ya kufanya kichwani mwake, kubwa zaidi ilikuwa ni kumpata Kamanda Amata ambapo mpaka dakika hiyo alikuwa akijua kwa uhakika mkubwa kuwa yupo katika nchi hiyo kwa kufuata ishara ya GPS ya simu aliyotumia. Hoteli aliyoipenda na kuichagua ni ile ya Light House, mwendo kama wa saa moja hivi kutoka uwanja wa ndege. Saa sita hivi akawasili katika hoteli hiyo, akapokelewa na kupata chumba.

Ndani ya chumba hicho kulikuwa na kitanda kikubwa na kiti kimoja chenye meza ndogo, akabwaga vitu vyake na kuifuata bafu, akajimwagia maji kisha kurudi ndani ya chumba hicho. Saa ya ukutani kamwashiria kuwa ni karibu saa saba usiku, Chiba hakuwa hata na lepe la usinginzi.

Maadam nipo hapa, lzima kamanda apatikane! Akawaza wakati akiwasha laptop yake na kuanza kuweka hai mtandao yake anayoijua mwenyewe. Safari hii alipoitafuta ile namba hakuipata hewani hivyo hakuweza kujua ni wapia au upande gani ambao mtu wake atapatikana, akaachana na hilo na kuendelea kup-ekua hiki na kile mpaka usingizi ukampitia mezani hapo.

Asubuhi kulipokucha kabla ya kufanya chochote, kwanza alifungua tena kompyuta yake na kutafuta uelekeo wa namba ile ambayo Amata allitumia siku mbili nyuma. Haikumsumbua, baada ya kuingia kwenye mtandao wa simu za nchi hiyo na kuvunja kodi kadhaa za kizuizi, akafanikiwa na kugundua kuwa uelekeo wa namba ile ni mahalia panapoitwa Waterloo. Akazidi kuichimba katika mtandao ikamwonesha umbali na uelekeo mji huo. Shauku aliyokuwa nayo ilimfanya hata asitamani kupata staftahi. Moja kwa moja baada ya kujiweka sawa akafika mapokezi na kutafuta usafiri wa kukodi wa kuelekea huko aendako. Akapata gari za watalii na kuikodi.

“Muda gani kutoka hapa?” akamuuliza dereva.

“Ni kama saa moja na nusu hivi,” akajibiwa.

“Sawa, sasa twende kisha tutarudi baadae…” akamwambia na safari ikaanza kuelekea huko Waterloo, mji mdogo Kusini mwa Freetown. Ndani ya gari lile alikuwa ametulia kimya kabisa katika siti ya abiri akitazama mandhari ya nje, milima na misitu minene, vijiji na mambo mengine mengi. Mazungumzo machache tu yalitawala kati yao kama kulikuwa na ulazima. Saa moja na nusu haikuwa muda mrefu kwao, waliwasili katika mji huo mdogo na kusimama mahali.

“Hii ndiyo Waterloo… kama unavyoona ipo kandoni mwa mto mkubwa wa Lofa…” yule dereva akamwambia Chiba.

Chiba akaanza kucheka.

“Vipi mbona wacheka?” dereva akamuuliza.

“Mto Lofa? Sisi kwetu hilo jina ukimwita mtu lazima akufundishe adabu,” akamjibu huku akiinua tablet yake na kuangali uelekeo wa anakotaka kwenda.

“Nipeleke bandarini…”

Yule dereva akawasha gari na kuendelea na safari huku akipita katikati ya nyumba zilizochoka, barabara zenye matope na madimbwi makubwa ya maji.

Nilifikiri njia kama hizi ni kwetu Sumbawanga tu, kumbe hadi huku! Akawaza. Lile gari likasimama kando ya bandari ndogo na tayari watoto wanaouza samaki walifika dirishani kuchuuza biashara yao.

“Kaka hapa ndo’ bandarini, umesema mwenyeji wako anapatikana hapa?” dereva akauliza, Chiba akajifanya kama hajasikia nini kaulizwa akamwita kijana mmoja na kumuuliza.

“Unamjua mtu mmoja anaitwa Hamadou?” akamuuliza.

“Hamadou? Huyu mvuvi?” yule kijana akauliza ili kupata uhakika wa jibu atakalotoa.

“Ndiyo!” Chiba akajibu hata kama hakujua kuwa huyo mtu ni mvuvi.

“Ndiyo, hakuna mtu asiyemjua Hamadou hapa mjini, ni mtu mwema mwenye kumcha Mungu, na sasa yupo paleeeee, ile ni nyumba ya dada yake!” akajibu.

“Asante sana,” akamshukuru na kumpatia noti ya dola ishirini kisha lile gari likaenda mpaka kwenye nyumba ile.

Chiba akateremka na kubisha hodi kwa kuugonga mlango, ukafunguliwa na mwanamke mwenye sura ya mviringo iliyojaa nyama mashavuni mwake. Akaeleza shida yake na kukaribishwa ndani. Dakika tatu nne baadae hakuamini kumuona Kamanda Amata mbele yake, akainuka na kumkumbatia kwa nguvu mpaka kila mtu akawashangaa.

“Hamadou, huyu ni kaka yangu,” Amata akamtambulisha kisha akawatambulisha kwa Chiba. Baada ya maamkiano hayo, mazungumzo ya msingi yakafuatia.

Saa mbili zilizofuata, Chiba na Anata wakawa tayari kuondoka, dada wa Hamadou alishindwa kuficha hisia zake na kuangusha machozi. Amata akambembeleza na kumuahidi kurudi kumsalimu.

* * *

HOTELI LIGHT HOUSE – FREETOWN

“Pole sana Kamanda!” Chiba alimpa pole mara tu baada ya kufika katika chumba ambacho alipanga kwa ajili yake.

“Nimeshapoa, unajua ni baada ya kuwasiliana na wewe, juzi ndo nimejua kuwa nipo bado Sierra Leone, Chiba nimeingia mpaka kaburini,” akamweleza.

“Pole, mama yako mvi zimemwongezeka, Gina, yeye ndo akikukumbuka tu machozi, kwa ujumla tulichanganyikiwa, nimekuatafuta siku tano bila kulala kwa maana, kodi zako zote hazisomi,” Chiba akamwambia. Amata akavua shati na kumwonesha kidonda katika paja la mkono wake.

“Wametoa chip na kuiharibu vibaya, wameninyang’anya simu zote na kuzipondaponda, nikabaki mimi tu, mateso niliyoyapata, Chiba, acha kabisa nilijua siponi lakini Mungu mkubwa…”

“Umeokokaje?”

“Kuna marehemu alinisaidia maana sote tulikutana katika kaburi moja,” Amata akaeleza maelezo ambayo Chiba hata hakuyafahamu maana yake nini.

“Kaburini kivipi?”

“Wale jamaa wana kaburi ambalo mtu akifa wanamtupiamo, sasa walijua mimi nimekufa wakanitupia humo, na humondani nikakutana mtu ambaye alikuwa dakika zake za mwisho za kukata roho, huyu ndiye akaniokoa mimi. Alinipa ishara nichukiue mkanda wake, huu hapa!” akamwambia na kumpa ule mkanda, kisha akendelea wakati Chiba kauchukua ule mkanda, “alipokufa na mimi hali yangu ikawa mbaya sana, nikaufunga ule mkanda kinoni kumbe haukua mkanda wa kawaida bali ni rimoti ya bomu,” Amata akamwelezea Chiba kila kitu mpaka alipojikuta katika boti ya akina Hamadou.

“Mh! stori yako imekomaa braza!” Chiba akamwambia huku akiinuka na kumtazama jeraha lake la kisogoni.

“Nilipigwa na kitu kama nondo sijui panga, likanizimisha kabisa,” Amata akasema bila hata kuulizwa.

“Pole kaka, sasa hapa inabidi kufanya mpango wa kurudi nyumbani Tanzania kwanza,” Chiba akamwambia.

“Najua, ila hii kazi lazima iishe,” Amata akasisitiza.

“Ndiyo ila kwa sasa inabidi turudi, kwanza tukaufanyie checkup mwili wako kisha majukumu mengine yatafuatia,” Chiba akamwambia.

“Umesomeka!” Amata akajibu bila ubishi maana alijuwa kuwa Chiba ni mjumbe wa Madam S hivyo anachomwambia ndicho alichoshema Madam S.

“AU imeunda timu mpya ya upeleelezi katika hili…”

“Wamechemka!”

“Kwa nini?”

“Kaka huu mtiti mwingine, mimi nimefika tayari paleee ambapo wapo, kumbuka ile shughuli pale Dar, kumbuka lile timbwili kaka, mi nimefika huku nimejitoa sadaka na ndiyo hivi, sikuwa duniani kama siku tatu hivi na moja ya nyongeza.



MIEZI MIWILI ILIYOPITA

DAR ES SALAAM

BAADA YA MAUAJI yaliyotokea Angola na Ivory Coast kuutikisa Umoja wa nchi huru za Afrika, iliazimiwa kuongeza ulinzi kwa viongozi wake na ikawa hivyo. Kikao cha viongozi wa juu wa umoja huo kikapangwa kufanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Kilimanjaro, na ajenda kubwa ya kikao hicho ilikuwa ni kuhusu mgogoro wa kiutawala katika nchi ya Somali land.

Iliaminiwa kuwa Tanzania ni nchi ya amani na usalama wa hali ya juu hivy, kikao hiki kilitakiwa kuwakutanisha marais sita na mawaziri kama kumi hivi ambao ndiyo hasa walikuwa na maamuzi ya mwisho kabisa katika hilo. Wakati wao wakipanga mpango huo wa kukutana Dar es salaam, kulikuwa na makundi mengine mawili nayo yakipanga mikakati juu ya kikao hicho hicho.

Mara baada ya taarifa kufika Ikulu, Rais akaona ni vyema sasa kuviweka vikosi vyake anavyoviamini kabisa kiusalama tayari. Mara baada ya kuzungumza na Mkuu wa Jeshi, Polisi na wengine wote hasa makachero wenye pua kali za kunusa. Jioni ya siku hiyo alimwita Madam S katika afisi yake nyeti na kuzungumza juu ya ujio huo.

“Kwa ujumla wageni wa kidiplomasia watakuwkama ishirini na mbili hivi na wale top kabisa watakuwa marais sita na mawaziri wawakilishi watatu na wengien watakuja kadiri ya kazi zao” akamwambia.

“Selina! Unajua kilichotokea Angol na Ivori Coast naomba uwe makini na vijana wako katika yale maeneo nyeti,” akamsisitizia.

Madam S alibaki kimya akimsikiliza huku akikumbuka hisia kali TSA 1 juu ya mauaji ya Rais wa Angola na Waziri Mkuu wa Ivori Cost, sipendi vitu kama hivyo vitokee katika nchi yangu, hakikisha mnafanya kazi, unaweka watu wako na kumkamata yeyote atakayeonekana kutaka kuharibu mkutano huu, kwa sababu pia ndiyo utakaoamua mchakato wa uchunguzi wa vifo hivyo,” akasisitiza huku akiipigapiga meza yake kwa ngumi.

Mara baada ya kutoka katika kikao hicho, Madam S aliwatumia ujumbe wa maandishi vijana wake na kuwataka nyumbani kwake Masaki kwa kula na kunywa usiku wa siku hiyo. Lakini lengo lake lilikuwa hasa kuzungumza nao juu ya kazi hiyo ambayo inawakabili ndani ya saa sabini na mbili zinazofuata.

* * *

Usiku wa siku hiyo, TSA wote walikutana nyumbani kwa Madam S kama walivyoitwa, kweli jiko kubwa la kuoka nyama lilikuwa limekokwa moto huku yeye mwenyewe akiwa bize kuwekaweka mafuta ili nyama iwe tamu, nzuri na laini.

“Leo Madam umeamua, umetuwekea mavitu si ya kifala,” Amata akamtania.

“Ee mle mnywe maana kazi yenyewe hii tufanyayo haina guarantee watoto wangu…”

“Aaaa kabisa,” Chiba akadakiza.

Kama ni swala la pombe kwa vijana hawa halikuwa la kuwasumbua vichwa, walikuwa na uwezo wa kunywa mpaka asubuhi lakini pale wanaptaka pombe ziwatoke huwatoka, wanajua wao ni kityu gani hupenda kula ambacho huwafaya warudi haraka katika hali yao ya kawaida.

“Sasa- mama- anatupatia- neno- linaloendana- na- kinywaji- hiki….,”Scoba akazungumza kilevi kidogo kisha akajitupa kochini. Madam S akawakusanya vijana wake nao wakasogea kwa karibu sana ili kuhakikisha ni nini hasa mwanamama huyo anataka kuwaambia.

“Wandugu, mi nimewaita hapa tufurahi, lakini zaidi ya hilo pia nataka niwajuze juu ya kazi yetu ya mbele hapahapa mjini tumeombwa tuitupie jicho. Tunajua kuwa hata kama tusingeombwa hii ni moja ya kazi yetu lakini ka sasa ni agizo kutoka kwa mheshimiwa Rais, hatuna budi kuitilia mkazo…” Kawaambia nao wakatikisa vichwa.

“Mkuu hataki nchini mwake yatokee ya Angola na Ivory Coast, anataka tutupe jicho kila mahala ili tuweze kujua kama kuna hila yoyote,” akaongeza.

“Sawa, unajua tunafanya hii kazi bila kujua kwa undani kabisa kama muuaji wa hawa watu ni mmoja na anaweza kuwa tayari yuko nchini, sisi tutatazama kesho kutwa wakati yeye tayari kaingia muda mrefu anatutazama tu…”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“…sijamaanisha keshokutwa ndo tuanze kazi, tukitoka tu hapa ndo kazi hiyo ianze kila mmoja akae kwenye kona yake ya kawaida na tuendelee kuwasiliana.” Madam S akamkatiza Amata.

“Nikirejelea mauaji ya Rais wa Angola najaribu kujenga mahusiano, na nikitafakari ujio wa wajumbe wa juu wa AU hapa Dar’ nahisi muuaji keshafika, maana muunganiko naupata kwenye chanzo cha mauaji na ule ujumbe wa video ambao tumeuona. Anasema ‘nataka AU iachie kipande cha Somali land kijitawale’. Kichwa kinaniuma Madam, ila tuwe tayari kwa lolote siku hizo,” Amata akaongeza kusema.

“Ndiyo, na ni la msingi sana!” akamalizia kusema.

“Ila wanausalama wa Angola na Ivori Cost nawafikiria sana, yaani wameshindwa hata kupata fununu? Maana mambo haya katika kuyachunguza inabidi ucheze na pande mbili tu, wasije wakajaribu hapa, lazima tuishangaze dunia kama tunavyoishangaza kila siku” Amata akaongea huku wenzake wakitikisa vichwa kumuunga mkono.

* * *

Msako wa wauaji ulikuwa ukiendelea kimya kimya katika nchi hizi mbili; yaani Ivory Coast na Angola. Nchi hizi mbili kila moja kwa wakati wake na kwa mtindo wake ilikuwa ikihaha kila kona ya nchi kusaka nani alifanya haya. Angalau kwa Ivory Coast, walikuwa na picha ya video iliyonaswa na na CCTV za hoteli ile ikimwnesha mtu anayehisiwa na kupewa utambulisho wa jina ‘UP’ yaani Unknown Person. Zaidi ya hapo walikuwa na cha kuzungumza walau kusema ‘mtu huyo aliingilia chumba namba 660 na kuwalaza usingizi wapenzi wawili. Lakini kwa Angola ikawa ngumu kujua hata uelekeo wa muuaji ulikuwa wapi.

Usiku wa Siku hii Amanda Keller alikuwa akijiandaa kwenda Uwanja wa ndege kumpokea Martin Gupter ambaye alibaki yeye tu kuwasili Dar es salaam ili kutekeleza mauaji ya tatu kadiri ya matakwa ya mteja wao. Walichotakiwa kufanya wakiwa katika jiji hili ni kuhakikisha wanapata taarifa zote za mkutano kwanza, kama zitakuwa zimeenda vyema kwa mteja nwao wasi zoezi lihairishwe na litakuwa limeenda ovyo basi aliyekusudiwa auawe. Fredy tayari alikuwa jijini karibu siku nne nyuma na alishapanga mambo yake yote tayari kwa kumsaidia Martin kukimbia. Amanda Keller aliwasili uwanja wa ndege wa Julius Nyerere saa nne za usiku, saa mbili kabla ya Martin kuwasili na ndege ya KLM. Alikuja muda huu makusudi ili kuona kama mtego wowote uwanjani hapo, alichopaswa kufanya ni kumpokea mgeni wake na mara moja kumkuimbiza hotelini anakotakiwa kufikia. Nje ya gari lake aliangaza macho huku na kule akisaidiwa na taa za maegesho zilizokuwa zikirusha mwanga wa dhahabu na kufanya eneo hilo kupendeza. Akavuta hatu na kuufikia uwanja huo haswa katika eneo la kusubiria wageni naye akajichanganya na watu waliokuwa katika eneo hilo wakisubiri ndugu na jamaa zao.

Saa sita usiku ilipotimia, dege kubwa la KLM liliwasili na kuingia maegeshoni tayari kuteremsha watu walioabiri katika shirika hilo. Martin Gupter alikuwa mmoja wapo wa abiria hawa. Siku hii alivaa kanzu ndefu ya Kiislam kutoka Oman, mkononi alikuwa na tasbihi aliyokuwa akiizungusha zungusha kwa vidole vyake, mkato wa ndevu zake, kwa vyovyote ungekupa shida ya kumtambua kuwa si mwarabu, alijua kujibadili na alijibadili haswa. Moyo ulimshtuka sana aliposikia tangazo ya kwamba abiria wte waliokuja na ndege hiyo wasubiri ndegeni kwa dakika kama kumi au kumi na tano.

Mh! Hii sijawahi kuishuhudia. Akawaza hukua akiendelea kuhesabu tasbihi kana kwamba anajua nini huwa wanasema katika hiyo. Akainua simu yake na kutuma ujumbe mfupi kwa mwenyeji wake.

‘Tumeambiwa tusubiri dakika kumi na tano kisha tutateremka, vipi nipe habari za huko duniani’

‘Huku shwari, nipo nje nakusubiri, sijajua kama kuna tatizo au ni nini!’ akajibiwa.

Baada ya dakika hizo kukamilika mlango ukafunguliwa na mmoja mmoja akaanza kuteremka. Martin Gupter akazishuka ngazi akiwa katikati ya watu, akavuta hatua na kuingia ndani ya uwanja huo kwa ukaguzi. Baada ya kuonekana kuwa pasipoti na vibali vyake hazina mawaa yoyote, afisa uhamiaji akamruhusu kupita huku wengine wakisubirishwa kwa sababu hii na ile.

Saa saba hii, usiku mnene, TSA walikuwa wamewasili uwanjani hapo kwa kazi maalumu mara tu baada ya kuachana na Madam S. Walitakiwa kuanza kazi mara moja, wakakubaliana kuwa kazi ya kwanza itakuwa ni katika Uwanja huo maana kwa vyovyo ni asilimi themanini wageni huingilia hapo. Ijapokuwa walijiuliza kama mwenye nia mbaya atashukia Kilimanjaro itakuwaje, wakaamua kupiga ngumi kichakani.

“Tumechelewa kuingia kazini, lakini si mbaya, kama kuna mmuaji basi mjue huwa anaingia si chini ya saa kumi kabla ya kutekeleza kazi yake,” Amata aliwaambia kabla hawajafika uwanjani hapo. Na mara baada ya kuwasili wakaingia katika afisi ya usalama ambapo huwa wanaonana na mtu mmoja tu, ni yeye pekee anayewajua watu hawa na kazi yao ijapokuwa naye anafahamu tu kuwa ni wanausalama, hajui kiundani zaidi.

Lulu alikuwa nyuma ya kompyuta kubwa katika afisi hii ambayo mtu huweza kuona kila kinachotukia katika uwanja huo. Ofisi hii inayoshughulika na maswala ya usalama wa uwanja huo, huwa haiingiwi na mtyu mwingine zaidi ya watu watatu tu; yaani Lulu na wengine wawili lakini mwanamke huyu alikuwa mtumishi wa Usalama wa Taifa Tanzania na aliwekwa hapa makusudi.

“Tunaanza na KLM,” Amata akamwambia Lulu.

“Mnenembia mapema kuna ndege nyingi sana leo zimeingia ukizingati huu mkutano, aaaa waandishi wa matelevisheni, maredio, magazeti wameshuka siku hii, nahisi mahoteli yamejaa,” akamjibu Amata ambaye alikuwa tayari ameshachagua siti na kuketi, huku Gina akiwa upande wa pili.

“Unajua, hisia zangu zimenituma nije usiku huu, nimezitii…” akasema huku akitupia macho kwenye luninga ambayo iliunganishwa na mashine ya xray inayokagua mizigo kwa kupiga picha kwa ndani na kuweza mtu kuona nini na nini kipo.

“Waruhusu!” akamwambia. Lulu akapiga simu na abiria wakaanza kupita kwa ukaguzi, Lulu na Gina wakatingwa kutazama abiria hao mmoja baada ya mwingine kama kuna sura watakayoitilia shaka huku Amata akaitzama mizigo tu inaypita katika mashine hiyo.

Ni mzigo mmoja, uliokuwa katikati ya mingine uikamtia shaka kijana huyu ambaye macho yake na akili hufanua kazi kwa haraka sana.

“Stop!!” akamwambia Lulu, naye akabonya kitufe kimoja na ile mashine ikasimama. Opareta wa mshine ile akaendele kubonya bonya kitufe lakini mashine haikuwa inatembea, hakujua kama kuna sehemu itakuwa imesimamishwa la. Dakika chache, mashine ile ikaanza kutembea tena.

“Gina, anaglia ni nani anachukua mzigo huo hapo,” akamwonesha kwa kidole kwenye luninga kubwa, naye akaanza kukodolea macho kwa makini. Amata hakumwambia mtu kama nini amekiona katika mzigo huo ila alitaka kujua tu ni nani kaupokea. Kutoka kwenye luninga ile, gina alimwona kijana aliyevalia Kiislam akiuchukua mzigo ule pamoja na mingine kisha akaipakia kwenye kitoroli tayari kutoka nje.

“Anatoka nje!” Gina akmwambia Amata.

“Mfuatilie!” kisha akamtzama Lulu, “we mwanamke, kamera za nje zinafanya kazi?” akamuuliza.

“Ndiyo, zote mpaka za Barabarani kuleeee zinafanya kazi,” akamjibu.

“Gina!” akaita, “hakikisha unajua mpaka taxi gani kapanda au gari gani,” akamsisitizia na msichana huyo akahakikisha anatimiza hilo.

Huko nje, Martin Gupter alikutana na mwenyeji wake, Amanda Keller, wakakumbatiana na kwa bashasha na kunyonyana ndimi kwa sekunde kadhaa ikiwa ni moja ya njia ya kuwafanya watu waelewe kuwa hao ni wapenzi kumbe hamna chochote. Baada ya hapo wakakokotana mpaka kwenye maegesho na kuingia ndani ya gari alilokuja nalo.

“Kila kitu kipo sawa?” akamuuliza Amanda.

“Yes!” Amanda akajibu huku akilitekenya gari lile na kuanza kuondoka taratibu.

Huku ndani, kamanda Amata akainuka kitini, “Vipi kuna ndege nyingine international kwa sasa?” akamuuliza Lulu.

“Hamna, ni mpaka kesho saa sita mchana!”

“Ok, kama kawaida, ukimshuku mtu tupatie taarifa haraka, tupo kwenye hatari sana siku hizi,” Amata akamwambia mwanamke huyo huku akitoka na Gina.

Wakiwa kwenye ngazi za kuteremka chini, Amata akamsimamisha Gina na kumtazama usoni, “umefanikiwa?” akamuuliza.

“Yes!”

Wakaendelea kutembea mpaka chini, Amata akamwongoza Gina mpaka ndani sehemu ya kufikia wageni, akaenda naye mpaka dirisha ambalo wanahisi huyo mtu alipita kwa ukaguzi wa pasipoti. Hapo wakamkuta mwanadada mmoja mrembo tu ameketi akiendelea kuweka mambo yake vizuri na taarifa pia.

“Samahani afande!” Gina akamwambia na kumwonesha kitambulisho chake cha polisi.

“Sisi ni polisi wa usalama hapa Uwanjani, samahani, kuna mgeni kapita hapa kwako, ni kijana amevaa kanzu hivi….”

“Ameshika tasbihi mkononi?” akamalizia mwanadada huyo.

“Yes!”

“Enhe….”

“Tunahitaji taarifa zake ambazo umekusanya tafadhali,” Gina akasema huku tayari mkono wake ukiwa ndani ya kidirisha kusubiri kama ni karatasi atapewa au ni kitu gani.

“Taarifa za mtu ni siri, nafikiri unajua…”

“…ndiyo najua!”

“Kwa hiyo kuna karatasi ya kusaini kabla hujazichukua,” akamwambia.

“Lete nisaini, fasta fasta basi,” Gina akamwambia kisha akapokea hiyo karatasi na kuisaini, akamrudishia, yule mwanadada akapriti karatasi fulani na kumpatia.

“Asante sana, msalimie shemeji….” Gina akamtania huku akicheka.

Safari yao ikaishia kwenye gari lao, wakaingia ndani na kujifungia kimya, gina akiwa nyuma ya usukani na Amata katika kiti cha abiria. Akampa lile karatasi, akalipokea na kulisoma vizuri kabisa.

“Abdulah El Marik, miaka 27, kutoka Oman…” akatamka Amata.

“Madumuni ya safari!” Gina akasema, nambie tafadhali.

“Sawa boss nitakwambia sasa hivi… mmmm likizo kwa mke wake Fatma Mansoor wa Kinondoni, unalingine Boss?” akamtania. Gina alikuwa macho mbele muda wote.

“Haiingii akilini hiyo, mwanaume katoka Oman kuja kwa mkewe Tanzania, mh! Halafu anakuja likizo, hapo moja jumlisha moja tatu,” Gina akamwambia Amata.

“Kwa hiyo…” Amata akamwangalia Gina huku akiikunja ile karatasi.

“N’na mashaka na hilo…”

“Wamechukua gari gani?” Amata akauliza.

“Gari binafsi, Lexus jeusi short chasis!” akamweleza.

“Ok, twende tukalale shamba!” Amata akamwambia na mwanamke huyo akaondoa gari kwa kasi na kuingia barabarani kuelekea mjini. Safari yao ilikuwa ya kuelekea Kigamboni mpaka Gezaulole ambako jingo lao la siri, ‘Safe House’ au wao hupenda kuliita ‘Shamba’ lilikuwako.

“Tukalale? Au tukafanye…”

“Tukafanye nini…”

“Umeshaanza, tukafanye kazi he!”

“Utafanya kazi mwenyewe mi nalala!” Amata akajibu huku akifyatua kiti na kujilaza.

* * *

Amanda akaegesha gari kando ya Barabara ya Nyerere kwenye service road nje ya jengo la Quality Group.

“Kuna njia mbili za kutekeleza mauaji ya kesho…” Amata akamwambia.

“Ipi na ipi?”

“Ama kudungua au kutumia mikono,” akamwambia.

Martin akakaa kimya kwa sekunde kadhaa akitafakari hilo aliloambiwa, “Amanda! Nahisi kazi ya safari hii itakuwa ngumu sana…” akamwambia.

“Kwa nini?” Amanda akauliza.

“Lazima watakuwa wamejipanga sana, baada ya bosi kuwatumia ule ujumbe ni kama kawaamsha…”

“Of coz, ulinzi upo tight sana, nimeshuhudia kila aliyeingia, ni kweli, inabidi tufanye kazi, kazi ya akili…” Amanda akamwambia.

“Anyway, twende hotelini kwako tukayaweke sawa,” Martin akamwambia Amanda kisha gari lile likaondoka tena kwa kasi ileile kuelekea mjini.

* * *

HOTELI YA GOLDEN TULIP

AMANDA, MARTIN na FREDY walikuwtana pamoja ndani ya chumba hiki ambacho kwacho mwanamke huyu aliweka makazi. Walikuwa mkononi na saa kama thelethini na nne hivi kujua kama waue au waondoke.

“Hii ni ramani ya Dar es salaam!” Amanda akawaonesha baada ya kufanya tafiti na kujifunza mengi ya jiji hilo, na kufanikiwa kupata ratiba nzima ya mkutano siku hiyo, na orodha ya nani na nani watakuwepo.

“Ukumbi wa mkutano ni huu, unaitwa Nyerere Conference, upo mita chache sana kutoka State House. Hili eneo limezungukwa na majengo au taasisi za serikali tu na ziko katika mpangilio maalum ambao ni vigumu kufanya shambulizi kama tulifikilialo…” Amanda akaeleza.

“Unamaanisha nini…”

“Namaanisha kuwa hii kazi hapa si ndogo, inahitaji akili ya ziada…” Amanda akasema huku Fredy akiwa kabaki kimya.

Martin akamgeukia Fredy na kumtazama, “tutatorokaje?” akamuuliza.

“Usijali, tutaondoka kwa njia ya maji,” akamwambia.

“Umeandaa boti?”

“Usijali, tutaondoka tu,” Fredy akawahakikishia. Kisha wote wakarudi kwenye ramani ile na kuendelea kuichambua.

“Amanda! Nafikiri hapa ni pazuri sana,” akamwoneshea jingo ambalo lipo mkabala na ukumbi huo wa mikutano ambalo limetenganisha na barabara na majengo kadhaa. Wakaingia kwenye Google Map na kulitazama jingo hilo.

“Yes! Hii ni target nzuri sana ndugu zangu, kama ni kuua lazima hawa watatokea mlango huu, sasa tazama hili jengo kwenye picha hii… ni refu kuliko mengine… lina ghorofa kumi na nne, nikikaa juu kabisa nina uhakika Napata shabaha nzuri hasa wakati wanapiga picha…” Amanad akatikisa kichwa kisha akachukua ratiba na kuitazama.

“Hah! Umejuaje kama kuna kupiga picha?”

“Nishasoma!” akamjiabu.

Baada ya mazungumzo na majadiliano hayo mipango ikasukwa vyema, siku ya pili ilikuwa ni siku ya kupanga mambo tu ikiwamo kutega vyombo vya kunasa sauti na kuangalia jingo hilo jinsi lilivyokaa ili kama umbali utakuwa ni tatizo basi watumie mbinu nyingine.

* * *

Usiku ule, Amata, Gina na Chiba walikuwa mezani wakizungumza jambo bila kujua kuwa upande wa pili wa bahari kuna wengine nao watatu kama wao wakiwa na mwanamke mmoja nao waikuwa wkipanga hayo hayo.

“Unajua, lazima tuwe makini sana na huu ugeni, na inabidi tufanye kazi kwelikweli maana hawa wauaji ni wajuzi, hatujawahi kuwaona sura wala kupata wasifu wao, sasa hapa ni hatari sana, lakini mi narudia tena huyu mtu lazima tumchunguze…” Amata akawaambia wenzake.

“Umegundua nini?” Chiba akamuuliza.

“Sikiliza, kati ya mizigo yake kuna mmoja una bunduki kubwa, kwa harakaharaka hata kama sijaijua ni aina gani ya silaha naihisi ni Magnum 22 riffle,” akawaambia.

“Sure?” Gina akauliza.

“Yes! Huyu lazima kesho jua lisilale, tupate habari zake zote….”

“Amata! You are right!” Chiba akainua macho yake kutoka kwenye kompyuta na kmshtua Amata.

“Nini Chiba?”

“Abdulah El Marik, ambao nawaona hapa wote hawamechi…. Alama zake za vidole haziendani na jina, wala sura inakataa, huyu aliyejifananisha naye, tayari ni marehemu!”

“Kwa hiyo?” Gina akauliza.

“Tulale, kesho tutaanza nay eye,” Amata akamwambia.



Siku iliyofuata…

Ujio wa rais wa Gambia ulikuwa asubuhi kwa sababu siku hiyo hiyo alitakiwa kutembelea sehemu kadhaa za jiji. Barabara ya Nyerere ilifungwa kwa takribani nusu saa hivi na kusababisha jiji zima kusimama. Ulinzi ulikuwa wa hali ya juu, askari wa mbwa na farasi walikuwapo achana na wale wa kawaida na wasiovaa sare. Kila mtu alishangaa kwa nini rais huyu apewe uinzi zaidi hata ya yule wa kwetu! Hawakuweza kupata jibu kamili bali kubabiababia tu; labda kwa sababu mgeni, hapana ni kwakuwa ni Mwenyekiti wa AU, kila mmoja akasema lake.

Asubuhi ya siku hiyo wanausalama walikuwa wametingwa kuhakikisha usalama wa kiongozi huyo, ujumbe uliotumwa na Jaffer Bakhari uliwapa tensheni ya kuongeza ulinzi wa siku hiyo.

Upande wa pili wa jiji hilo, mita chache kutoka Ikulu ambako mgeni huyo angefikia, Kamanda Amata aliegesha gari nje ya geti la kuingia ‘Ofisi Ndogo’, akateremka na kuingai akatika ofisi hiyo ambamo alimkuta Madam S akiwa ametingwa na kazi huku akipokea simu hii na ile.

“Karibu!” bakamkaribisha Amata, “vipi mbona kama una ari ya bjambo fulani?” akaongeza swali.

“Of coz! Ni hivi, jana usiku kwa ndege ya KLM kuna mtu kawasili nchini ambaye tunamshuku kwa hatari zote. Sasa wasiwasi wangu asije kuleta madhara kwani mpaka sasa bado tunamfuatili nyayo zake. Naomba uwasiliane na watu wa usalama huko uwanja wa ndege na kwenye msafara wake ili wawe na tahadhari zote…”

“Kwa nini unamhisi?” Madam akamuuliza.

“Katika begi lake kuna Magnum 22 rifle, halafu katumia sura ya bandia, na mwenye sura hiyo tumegundua kuwa ni marehemu…”

“Nyie vijana mshafika mbali hivyo!”

“Umetuambia tufanye kazi na ndiyo tulianza jana ile ile…” akamwambia.

“Sawa, hiyo ni habari njema na inabidi adhibitiwe kabla hajaleta madhara..” Madam S akasema hivyo huku akiwa tayari keshaweka simu sikioni na kuwasiliana na wahusika. Taarifa hiyo iliwasha moto usiotegemewa, wanausalama wakahaha wakipita kila jingo karibu na barabara ambayo rais huyo anategemewa kupita.

“Madam S akamwangalia kijana wake…”

“Una akili za ajabu sana, ina maana kama usingechukulia maanani maagizo yangu ya jana basi labda ntu huyo angetuletea madhara ambayo hatukuyategemea,” akasema.

Huko uwanja wa ndege hali ilikuwa tafauti baada ya kupata ujumbe huo, ilibidi wanausalama wajipange upya, baadhi ya wanajeshi wakachukua nafasi kwa ombi maalumu wakashika doria hapa na pale, wakitumia darubini kubwa na zenye nguvu kutoka juu ya majengo wakitazama kila mahali.

Saa mbili baadae, wanausalama wakaufikisha msafara wa rais huyo salama kabisa Ikulu, wakati huo Amata na Madam S walikuwa ndani ya gari karibu kabisa na kona ya mwisho ya kuingia Ikulu.

“Wamefika salama, asante Mungu!” Madam S akashusha pumzi ya nguvu.

Amata akainua simu na kumpigia Gina kujua upande gani wa jiji alipo.

“Nipo, Tazara junction!” akajibu.

“Fika ofisi ndogo mara moja!” akamwambia na kisha akashuka na kuliacha gari la mwanmama huyo.

“Kwa hiyo….” Madam S akataka kujua.

“Nitakutafuta jioni nikupe habari, naingia kazini kumsaka mshenzi yule,” akamjibu. Kamanda Amata mara baada ya kuachana na bosi wake akarudi ofisi ndogo na kuanza kupanga kipi cha kufanya. Nusu saa baadae Gina akaingia na kumkuta Amata akiwa anamsubiri. Alipomwona tu akasimama na kumshika mkono.

“Wapi sasa?” akauliza.

“Kazini, inabidi tumsake yule jamaa,”

“Sasa tunaanzia wapi?”

“Hata mi sijui,” Amata akajibu huku wakitoka na kuingia ndani ya gari tayari kwa safari.

* * *http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Katika hoteli ya Al Huruba, Kariakoo, Martin Gupter alishituka usingizini, akatazama saa yake, tayari ilikuwa imetimu saa nne asubuhi, akainuka na kuwasha TV. Alichokutana nacho kilikuwa ni matangazo ya moja kwa moja kutoka Ikulu juu ya makaribisho ya ugeni huo mkubwa.

“Ameshafika!” akajisemea na kuingia maliwato, akajimwagia maji na kubaki Martin Guter halisi siyo wa kujibadili sura kama ilivyokuwa jana. Akachukua simu yake na kumpigia Amanda kutaka kujua yuko wapi. Mwanamke huyo akamwambia kuwa yupo mitaa ya katikati ya jiji akitalii na kusikiliza hili na lile kutoka kwa wananchi.

“Endelea kulala, nahitaji kukuona nina habari ya kushangaza kidogo,” akamwambia mgeni wake na kukata simu.





ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog