Search This Blog

Friday 18 November 2022

KUFA NA KUPONA - 1

 






IMEANDIKWA NA : ARISTABLUS ELVIS MUSIBA (A.E MUSIBA)



*********************************************************************************



Simulizi : Kufa Na Kupona 
Sehemu Ya Kwanza (1)


 Karatasi za Siri



Ilivyo ni kwamba mimi siku za Jumapili hulala mpaka saa tatu au saa nne. Na kama huamini hiyo si shida yangu. Ilikuwa Jumapili nyingine. Usiku wa jana, yaani Jumamosi, nilikwenda kwenye dansi na rafiki yangu mmoja msichana. Tulirejea nyumbani mnamo saa tisa na nusu za asubuhi. Kutokana na uchovu mwingi ulionielemea nikafahamu wazi kwamba Jumapili hii nitaamka kama saa tano hivi. Lakini utastaajabu nikikwambia kuwa Jumapili hiyo ilinibidi niamke saa kumi na moja alfajiri!



Kengele ya simu ililia mnamo saa kumi na moja, na miye nilikuwa nimelala saa moja tu hivi. Nilipuuza kuichukua kwani nakueleza nilivyochukia, Mungu ndiye anayejua. Iliendelea kulia na kulia, mwishowe nikaona nisipoijibu pia nisingeweza kulala kwa sababu ingaliendelea kuniudhi. Huyu binti aliyekuwa amelala karibu na hii simu naye aliamka, akaniomba afadhali niijibu. Basi kwa shingo upande, nilimwambia huyu binti anisogezee. Yeyote yule aliyekuwa amepiga hii simu nilikuwa mpaka sasa nimechukia kiasi cha kwamba angalikuwa karibu ningalimwuma.



"Hallo, huyu ni Chifu." Nilisikia sauti ikisema.



Usingizi ulipotea papo hapo, nikajua kuna jambo, maana, S, anapojifahamisha kwa jina la Chifu jua kuna kazi, na kazi kubwa. "Halo, huyu ni Willy. Chifu mbona unapiga simu wakati kama huu? Nadhani ingefaa uwe kitandani, la sivyo utazidi kuzeeka upesi, kwa mtu wa makamo kama yako, " nilimjibu.



"Sikiliza Gamba, hapa ninapopigia simu ni ofisini, na wala si nyumbani-kitandani kama ambavyo ungalifikiria. Na miye nakuhitaji hapa ofisini mnamo nusu saa bila kuchelewa. Kuna jambo la muhimu na la haraka, hili si ombi ila ni amri, asante sana," alimalizia Chifu.



Nakueleza, hakika kweli, kuna wakati mwingine ninapochukia hii kazi yangu, lakini hata hivyo kwa mtu kama mimi nipendaye visa, nikiwa nasikia kuna jambo kubwa kubwa basi moyo nami huwa unanidundadunda ukiniambia nenda, huenda mara hii kuna visa zaidi.



Della ambaye ndiye msichana niliyekuwa naye hakupenda kuniona naondoka saa kama zile. Akaniambia, "Willy hii ndiyo sababu nakuchukia. Sasa karibu tena uende kwenye masafari yako ya ovyo ovyo, hasa unapoitwa na hilo lijanaume linaloitwa liChifu. Kweli kama mara hii ukikubali kwenda miye naweza kufa."



Nilimjibu Della nikisema, "Wajua kabisa ya kwamba hii ndiyo kazi yangu, ndiyo inayonipa unga, mboga na starehe za kila aina. Nisipofanya hizi safari, itakuwa kama wewe usipoenda ofisini."



Kwa sababu Della ni msichana mwenye hekima alinyamaza na kuelewa nimesema nini. Kumwacha msichana huyu, na asubuhi kama hii amelala kitandani, na miye nikakimbia ofisini, ati kusudi nikapige ripoti kwa Chifu, moyo wangu ulidunda mara nyingi zaidi. Kama ningehesabu wenda mapigo yangefika tisini kwa dakika moja. "Nitarudi mapema baada ya kumaliza shughuli na Chifu," nilimwambia Della.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Nilifungua mlango, nikaangaza nje maana kulikuwa bado giza giza. Macho yalipozoea nikafunga mlango kwa nyuma, nikaenda kwenye gari langu. Nikaingia ndani na kuliwasha gari hilo. Kutoka kwangu ambako ni Upanga, mpaka ofisini kwetu ni mwendo wa dakika kumi. Kwa sababu wakati kama huu hakuna magari mengi nilitegemea kuchukua dakika tano hivi. Ingawaje ni kawaida ya Dar es salaam kuwa na joto jingi, asubuhi hii kulikuwa na baridi sana. Nilitia gari moto, nikashika barabara ya United Nations moja kwa moja mpaka Jangwani kwenye taa za 'traffic.' Nikaona hakuna gari ingawaje zilikuwa haziniruhusu kupita. Lakini nilienda tu. Nikaingia barabara ya Morogoro hadi Independence Avenue.



Nilipoingia Independence Avenue, niliona gari moja inakuja kwa nyuma. Na ilionekana kama kwamba ilikuwa imesimama katika barabara ya Morogoro wakati nikipita, kwa hiyo nikapunguza mwendo, na hiyo pia ikapunguza. Miye nilikuwa sipendi mtu yeyote ajue kuwa nilikuwa nikienda ofisini, saa kama zile. Na kwa nini hilo gari likawa linanifuata? Hiyo ndiyo pia nilikuwa sitaki. Nakwambia, kwa sababu nilishafutwa na magari mengi, mara moja tu naweza kutambua kuwa lile gari linanifuata hata anayenifuata awe mjanja namna gani. Wakati huu nilikuwa nimebakiwa na dakika kumi tu kuripoti kwa Chifu.



Nilikata shauri kurudi mara moja nikaone nani aliyekuwa ananifuata. Basi nilipiga kona na kuanza kurud. Hilo gari lilipoona nimerudi, likatia moto kuja kwa kasi sana. Likanipita na kwenda mwendo wa kama maili mia moja kwa saa. Dereva wa hiyo gari alikuwa amejifunga shuka. Alikuwa amevaa miwani mweusi ya jua. Nikabahatisha kuwa, huyo alikuwa mtu ninayemfahamu, hivyo alivaa ili kusudi nisiweze kumtambua. Gari lake lilikuwa aina ya Datsun 160 SSS lakini alikuwa ametoa sahani ya namba.



Nilikata kona tena nikaendelea na safari yangu mpaka ofisini. Niliendelea mbele kidogo ya ofisi kusudi nione kama hilo gari lilikuwa karibu hapo. Ilionekana huyo jamaa alikata shauri kwenda zake. Nilianza kupanda juu ya jumba ambalo ndimo zilimo ofisi zetu hapo Independence Avenue karibu na jengo la Bima ya Taifa. Ilikuwa tayari saa kumi na moja na nusu. Niligonga kwenye mlango wa ofisi ya karani wa Chifu. Nilisikia sauti ya Maselina ikinikaribisha.



Nilifungua mlango na kuingia ndani. Nilimuhurumia sana Maselina maana naye alionekana mwenye usingizi mwingi. Nilipomuuliza alifika saa ngapi ofisini alinieleza kuwa Chifu alikuwa amempitia nyumbani kwake huko Magomeni Mikumi, yapata saa kumi hivi, wakati yeye alipokuwa amefika kutoka 'Afrikana Hoteli' ambako alikuwa ameenda kustarehe na rafiki zake. Akazidi kunieleza kuwa lazima kulikuwa na jambo kubwa sana kwani Chifu alionekana hana furaha kabisa.



Kweli Maselina alifaa sana kuwa karani wa Chifu, maana alikuwa msichana mwenye bidii sana ya kazi. Hata mimi nilimpenda kwa ajili ya bidii zake na pili alikuwa na umbo la kupendeza. Alizidi kunieleza kuwa Chifu alikuwamo ndani akiningojea. Maselina alimpigia simu Chifu na Chifu akamwambia aniambie niingie. Basi niligonga kwenye mlango ulioandikwa "MKURUGENZI WA UPELELEZI." Nilisikia sauti ya Chifu ikisema, "Ingia ndani Gamba."



Nilipoingia ndani nilimkuta Chifu anavuta mtemba. "kaa chini," aliniambia. Sura yake ilionyesha kama kwamba kulikuwa na jambo ambalo hakulipenda. Alikaa kama dakika kumi hivi akiniangalia tu bila kunieleza neno. Hata miye mwenyewe nilijisikia sina furaha hata chembe. Kisha Chifu alitoa mtemba wake kwenye mdomo, akakung'utia majivu ya tumbaku katika sahani la majivu. Akaanza kutia tumbaku mpya. Halafu akainua macho yake na kuanza kusema,

"sikiliza kwa makini sana tafadhali maana sitaki kuwepo makosa yeyote ambayo yanaweza kuleta hatari. Habari niliyonayo ni muhimu sana, hivyo kwamba, kosa la mtu mmoja tu, linaweza kuleta maangamizi ya Afrika nzima."



"Mnamo usiku wa manane, nimepokea simu nyumbani kwangu ikitoka kwa mkubwa wa Polisi. Mkubwa wa Polisi alinieleza ya kwamba, ofisi moja ya wapigania uhuru imebomolewa. Na kwamba karatasi fulani za siri zimechukuliwa." Alipofika hapo Chifu alionekana hana furaha katika kutaja neno hili 'zimechukuliwa.' Aliendelea kusema, "Na polisi wanafikiri kwamba jambo hili limefanyika kati ya saa nne usiku na saa tano. Askari Polisi aliyekuwa akilinda amekutwa amekufa kwa kupigwa risasi tatu kifuani. Polisi walifika hapo ofisini yapata saa tano kamili, baada ya kupigiwa simu na mtu mmoja aliyeiona hiyo maiti ambayo ilitupwa barabarani. Mtu huyo alikuwa akitoka dansini akielekea nyumbani kupitia mtaa wa Nkurumah.



"Polisi walifika na Dakitari. Daktari alieleza kwamba huyo askari alikuwa amekufa yapata saa moja iliyopita, ambayo ilionekana ilikuwa saa nne. Mkubwa wa wapigania uhuru alifika baada ya kupigiwa simu na akachunguza vitu vilivyopotea. Ilionekana kwamba kila kitu kilikuwemo ila kabati moja la chuma ambamo mlikuwa na karatasi za siri, kufuli la kabati hilo lilifunguliwa kwa kutumia bastola .45. Karatasi hizo zilizochukuliwa ni za maana sana kwamba lazima 'kwa njia nzuri ama mbaya' zipatikane. Maana zisipopatikana, zinaweza kuleta maangamizi kwa wapigania uhuru na kwa nchi huru zote za Afrika."



Alipofika hapa mimi nilisema, "ingefaa unieleze jinsi ninavyohusika katika mambo haya, maana mpaka sasa bado inaonekana hakuna jambo au kiini cha kuweza kuzipata iwapo hawamjui mtu yeyote aliyehusika na mambo haya."



Chifu hakusita kupanua midomo kunieleza, "baada ya kuelezwa yote haya, imeonekana kwamba. Na pia wakuu wa serikali wanafikiri kuwa wizi wa karatasi hizi, Ureno na Afrika ya Kusini ndiyo wako nyuma ya mambo yote haya, pia Indonessia. Lakini watu waliofanya au waliozichukua hizo karatasi ni watu au majambazi wa papa hapa Afrika ya Mashariki. Maana kutokana na wizi wenyewe ulivyotokea, imeonyesha kwamba ni watu wenyeji wa Afrika ya Mashariki tu wanaweza kuendesha wizi huu.



"Mimi sasa ninavyofikiria ni kwamba hizo karatasi zina mambo yote jinsi wapigania uhuru wanavyoweza kufaulu katika mambo yao. Kwa hiyo wakafanya jitihada wazipate, lakini hawakuweza, maana wapelelezi hao wote wamekamatwa kama unavyojua. Hivyo wakaona jambo wanaloweza kufanya ni kuwafuata majambazi katika Afrika Mashariki ambao haja yao kubwa ni pesa. Sasa basi, hao watu wakafuata hao majambazi na kuwambia kuwa watalipwa pesa kiasi kikubwa. Na hapo ninavyofikiriwa. Majambazi wakakubali kufanya hivyo.



"Zaidi ya hayo," aliendelea Chifu, "hao majambazi hawajali kama wapigania uhuru wanashindwa ama wanashinda. Na wala hawaoni hatari za mbele kwa nchi zote za Bara la Afrika. Kweli, hao majambazi ninavyofikiria kuwa ndiyo wamefaulu.



"Sasa hapo ndipo sisi tunaingia katika habari hii. Na sasa sikiliza kwa makini. Wakuu wa Serikali wamekaa na kufikiri usiku huu huu na kuona watupe sisi kazi hii, na ni lazima tufaulu ama sivyo bara zima la Afrika litaumia si Tanzania wala Zambia wala Ethiopia wala Kenya zitakazoumia pekee. Wala si Msumbiji na Rhodessia na Angola peke yake. Kwa hiyo nimekuita wewe na utaondoka leo hii kwenda kwenye tume hii. Ninavyofikiria ni kwamba karatasi hizo hazijatoka katika Afrika Mashariki, maana Polisi katika nchi zote wameishafahamishwa na kuna ulinzi mkuu katika mipaka, viwanja vya ndege na mahali penginepo.



"Hao majambazi wanajua kwamba Serikali itachukua hatua kuzitafuta hizo karatasi kwa njia nzuri ama mbaya watajaribu kuwapa wanaohusika upesi iwezekanavyo. Lakini nadhani hawatazitoa mpaka wamepokea fedha yao. Lakini lazima ujue kuwa makundi ya majambazi yana akili sana wanangojea sisi tuanze kushughulika kusudi wajue kama kweli tunaweza kuwafikiria wao. Watakapoona kuwa tunawashutumu, mara moja na wao, wataanza kupambana nasi, maana hawatakubali kupoteza hiyo fedha. Hapo ndipo maisha yatakuwa magumu maana itakuwa ua au uawa. Na huenda wakasaidiwa na majasusi toka Ureno, Afrika Kusini na Rhodesia.



"Na pia nilifikilia kuwa, hao majambazi watapanga mahali pa kuonana na hao watu ili wabadilishane hivi vitu. Na lazima wapelelezi wa nchi hizi ndiyo watatumwa na Serikali zao kuja kuonana na hao majambazi. Hatari nyingine ni kuwa hao majambazi lazima wawe na majina ya wapelelezi wetu maarufu, na wewe ukiwa nambari moja kwenye orodha hiyo. Sasa ninafikiria kuwa ofisi kuu ya majambazi hao iko Nairobi. Kwa hiyo utaondoka hapa kwenda Nairobi, leo hii saa tatu unusu na ndege ya shirika la ndege la Afrika Mashariki.



"Vyeti vyote vya kusafiria viko tayari. Huenda itakubidi usafili mpaka Afrika Kusini au Ureno au Rhodesia ikiwa lazima. Mambo ya safari katika nchi hizo pia yako tayari. Ukiona ni lazima kusafiri katika nchi hizo usisite. Jina lako tangu sasa ni "Joe Masanja," na kazi yako ni uandishi wa habari juu ya maonyesho ya mavazi. Maana tangu kesho maonyesho ya mavazi yataanza kote ulimwenguni. Upashanaji wote wa habari kati yetu katika kazi hii, utajulikana kama "Kufa na Kupona." Na pia nakupa hiki cheti ambacho kimetolewa na Serikali, kikikuruhusu kuua kama ni lazima. Nakutakia mafanikio mema. Mungu akusaidie ila nakuonya usihusiane sana na mwanamke, na katika hii safari usimwamini mwanamke yeyote."



Chifu alimalizia kunieleza, lakini bado niliona mambo yote hayo ni kama muujiza. Kwani hakukuwa hata na chambo cha kuanzia. Ilikuwa kwamba nitaenda Nairobi bila hata kuwa na fununu ya mtu ambaye anaweza kuhusika habari yote niliona kama ya mwendawazimu. Kweli ilikuwa uendawazimu mtupu. Kisha nikamuomba Chifu kama angaliweza kuniruhusu kuuliza swali, naye akakubali.



Nilimuuliza, "kuna mtu yeyote ambaye anaweza kunisaidia huko Nairobi?"



"Nitapata jina la huyo mtu mnamo saa mbili na nusu asubuhi hii, na kama pia kutakuwa na maelezo yoyote zaidi nitakupa wakati huu."



Nilitoka ofisini kwa mkurugenzi wa upelelezi, na kufungua mlango. Nilimkuta Maselina amelala kwenye meza: Nikamgusa hakaamka. Akaniuliza ilikuwa ni saa ngapi. Nikamweleza ilikuwa saa kumi na mbili unusu. Akaniomba nimweleze kwa kirefu palikuwa na nini. Lakini sikuwa na muda, kwani ilikuwa inanibidi nijitayarishe upesi iwezekanavyo, nipate ondoka saa tatu.



Nilimweleza kwa kifupi tu mambo yalivyokuwa. Maselina akaniambia, "Willy, kweli safari hii mambo ni mengine, na kesi hii inaonekana imejisokota vibaya sana. Lakini naamini unaweza ukaisokotoa na kurudi salama Mungu awe nawe."



Nakwambia kama mtoto huyu angalikuwa anakuaga wewe, walahi usingefanya safari, maana utadhani badala ya kukuombea usalama, anakuombea maafa! Maana hiyo sauti yake ilikuwa mno mbichi mbichi. Nilimwaga Maselina.



Nilitoka nje nikakuta kulikuwa kumeishapambazuka. Nikaingia katika gari langu, huyoo Upanga. Mitaani bado hakukuwa na watu maana kumbuka kuwa hii ni Jumapili. Nilipofika nyumbani kwangu nilimkuta Della bado amelala. Lakini baadae aliponiona tu, jambo la kwanza kuniuliza ni kama nitaondoka. "Naondoka mnamo saa mbili zijazo."



Della alianza kulia, na huyo mtoto anapolia, ndipo anakuwa mzuri kiasi cha ajabu. Utadhani mwelekevu ambaye Shaaban Robert anamzungumza katika kitabu chake cha 'Adili na Nduguze. Kama hujakisoma miye Willy nakuomba ukakisome ndipo utajua Della ni msichana mzuri wa kiasi gani.



Nilimbembeleza Della na kumwambia, "Usijali sana. Safari si mbaya sana, na nitarudi muda si mrefu." Lakini moyoni nilijua hii safari ilikuwa "HATARI TUPU!"



Della aliamka akaanza kutengeneza kahawa, wakati mimi nikifungasha vitu vyangu vya lazima. Muda mchache kijana mmoja alibisha hodi mlangoni. Nilipomuona nikafahamu kuwa alikuwa mfanyakazi ofisini kwetu. Daudi alikuwa ametumwa na Chifu kuniletea kamera moja ya gharama sana, ambayo ningetumia kama mwandishi wa habari na mchukua picha za maonyesho ya mavazi. Pia alibeba bastola mbili zote " automatic .45." Visu sita na vitu vingine ambavyo ningeweza kuvitumia safarini.



Pia alinieleza kuwa Chifu alikuwa amekata shauri niende pamoja na ofisa mwingine wa upelelezi, kwa jina la Sammy Rashidi. Huyu kijana nawambieni nyie kuwa ni mwamba, maana katika kazi yetu hii kila siku ni nambari mbili akinifuata mimi. Na mara nyingi ameponyesha maisha yangu. Alishawahi kushinda mashindano ya kutupa visu katika mashindano ya Jumuia ya Madola. Ukiwa na bastola na Sammy akiwa na visu, jua umekwisha kazi!



Kusikia Sammy anakwenda na mimi, Moyo wangu ulipata furaha kidogo. Daudi alinieleza kuwa Sammy atakwenda akitumia jina la Athumani Hassani. Kazi yake itakuwa msaidizi wangu katika mambo ya kuchukua picha, na yeye ndiye atakayekuwa mchukuaji picha, na kwamba tutaonana naye kiwanja cha ndege cha hapa Dar es Salaam saa tatu.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Sasa ilikuwa saa moja na nusu, Della alikuwa tayari ameweka kahawa, mayai na mkate. Miye nilikuwa nimemaliza kufungasha vitu vyangu. Nilikuwa nangojea tu habari zaidi kutoka kwa Chifu. Tulikaa mezani na Della na kuanza kunywa kahawa. Nilizidi kumbembeleza Della, "Usijali sana juu ya safari yangu. Na kama mola akipenda tutaonana tena."



Ilipofika saa mbili kamili, simu ilisikika. Nikaenda kuijibu, na kama ilivyotegemea, ilikuwa inatoka kwa Chifu. Chifu alisema, "Gamba sikiliza. Nairobi mtaonana na Ofisa mwingine wa Upelelezi aitwaye John Mlunga. Huyu ni kijana tunayemuamini sana. Nadhani mlishawahi kuonana. Yeye aliishafika Nairobi toka Kampala asubuhi hii. Atakungojea saa nne asubuhi katika Hoteli ya Fransae huko Nairobi. Inaonekana yeye anafununu kidogo kuhusu hii habari mpaka wakati huu. Maana anajua mambo mengi sana ya hapo Nairobi baada ya kufanya kazi hapo kwa siku nyingi akipambana na majambazi wa hapo kwa muda mrefu. Sasa tayarisha kila kitu uondoke. Nakuombea safari njema."



Baada ya kupata habari zote hizi kwa Chifu nilionelea sasa niondoke kwenda zangu kwenye kiwanja cha ndege. Ilibidi Della anisindikize mpaka kwenye kiwanja ili apate kurudi na gari. Sikuwa na mzigo mkubwa sana, kwani huwa nina mfuko mmoja wa ngozi ambao nikiufunga unaonekana mdogo sana lakini ndani yake unaweza kubeba hata ngamia! Della alitia gari moto tukaondoka. Niliangalia nyuma kuiangalia nyumba yangu na sehemu ya Upanga kwa makini sana. Sijui ilikuwa mara ya mwisho kuiona ama nitaiona tena, huo ulikuwa ndiyo wasiwasi wangu.



Nilionelea nipite kwanza mtaa wa Nkurumah nikaone hilo jengo lililobomolewa, kwa sababu nilikuwa bado na dakika ishirini za kupoteza kabla sijafika kwenye kiwanja cha ndege. Na mwendo wa kutoka mjini mpaka kiwanja cha ndege. Ikiwa Della anaendesha ni dakik tano, kwani huyu msichana anafahamu kuvuta gari.



Nilipofika kwenye hilo jengo, nilimwacha Della ndani ya gari nikamwambia, "usitoke garini humu ila uwe ukiangalia ikiwa kuna mtu yeyote anayeonekana na wasiwasi wa kuiona hii gari hapa."



Wakati huu watu wengi walikuwa wamekusanyika kwenye hilo jengo, kwa hiyo ilikuwa rahisi sana kuchunguza mambo fulani fulani bila mtu kuwa na wazo lolote juu yako. Polisi walikuwa wanasukumasukuma watu wasikaribie sana, hata mimi nilianza kusukumwa lakini polisi Inspekta mmoja alivyoniona alinichukua na kunionyesha kila kitu. Jambo moja nililofikiria ni kwamba hao watu waliobomoa hili jengo walikuwa wakifahamu kabisa kuwa hizo karatasi za siri zilikuwa kwenye hili kabati la chuma, maana la sivyo, wangalikuwa wamejaribu kupinduapindua na kutafuta tafuta kila mahali. Lakini vitu vyote hata wino katika vidau, haukuwa umemwagika japo tone moja hii inaonyesha kuwa walikuja moja kwa moja bila kugusa kitu kingine chochote, na kupiga kufuli la kabati kwa risasi na kuchukua karatasi na kwenda zao. Pia inaonekana haikuwachukua muda mrefu.



Hili jambo ambalo nimekueleza hapo juu, linanipa wazo. Na kama wewe pia ni mtu mwenye kufikirlia kama miye Willy nadhani tayari umepata wazo ni kwamba hizi karatasi zilikuwa zikifahamika kwa watu wachache sana. Na kama hata zilijulikana kwa wapigania uhuru kuwa zipo, wachache walijua zipo wapi. Kwa hiyo ingawaje hao majambazi walijua zipo, wasingeweza kujua mahali gani zilipo, mpaka wameambiwa na mtu anayejua zaidi juu ya karatasi hizo. La sivyo wangalitafuta kila mahali kabla ya kuzipata. Hivyo tungalikuta vitu vimevurugwa vibaya sana. Kama una kichwa cha kufikiria nadhani umejua nina maana gani.



Baada ya kupata fununu fununu, na kufikiria mambo mawili matatu, niliondoka hapo mahali na kurudi kwenye gari ambamo Della alikuwa akiningojea. Della aliniambia, "Sikumuona mtu yeyote ambaye alionekana kuwa na wasiwasi juu ya gari hii. Ila tu niliona gari moja aina ya Dutsun 1600 SSS, dereva wake alikuwa amevaa shuka na miwani myeusi. Dereva huyo alinitupia macho kidogo tu."



Nadhani hiyo habari ya Della inakupa wazo jingine kwani hilo gari ndilo lililokuwa likinifuata wakati nikienda ofisini kwa Chifu. Della alivuta gari moja kwa moja mpaka kiwanja cha ndege ambako tulimkuta Sammy akiningojea kwa hamu. Nilimwaga Della kwa kumbusu kisha akarudi zake hali machozi yakimtoka.





Wasiwasi



Sammy alikuwa ameelezwa kwa kifupi na Chifu juu ya habari yote, hivyo aliomba nimweleze kwa urefu mambo yalivyo. Wakati wote huo hata Sammy, hakuwa akiona dalili yoyote ya kupata mwangaza wa jambo hili. Wote tulionekana vibuda.



Hapo uwanja wa ndege palikuwa na ukaguzi mkali sana. Lakini kwetu siye Chifu alikuwa amefanya mipango yote, kwa hiyo tulipita moja kwa moja mpaka kwenye ndege. Wakati huo nilikuwa bado najaribu kufikiri jambo hili na lile, kama naweza kutoa jambo kamili lakini wapi. Yule mtu mwenye shuka na miwani myeusi alikuwa akija kwenye mawazo yangu kila wakati. Mambo niliyofikiria kwenye lile jengo lililobomolewa pia yalikuwa yakinijia mara kwa mara. Nikamweleza Sammy kila fununu, au jambo lolote nililofikiria linaweza kutusaidia. Sammy naye akanipa mawazo yake.



Ilipofika saa tatu u nusu ndege iliondoka. Tuliiangalia Dar es Salaam kama kwamba hatutaiona tena. Hakuna aliyeamini ataiona tena. Wasafiri wenzetu walionekana kuwa wachovu wote kama sisi tulivyokuwa, kwani kama unavyojua ni Jumapili asubuhi. Mie nadhani ndiye niliyekuwa mchovu kushinda wote. Kwa hiyo nilimwambia Sammy awe macho wakati mimi nikijipumzisha kidogo maana katika kazi yetu hii huwezi kujua ni nani adui na nani rafiki. Wote ni maadui zetu mpaka tutakapohakikisha wenyewe mia kwa mia, ni nani rafiki yako. Na pia nilimweleza kama kukitokea kitu chochote ambacho atakishuku aniambie. Kwani nilijua mchana huo Nairobi kungekuwa na shughuli kubwa sana.



Sammy aliponiamsha niliona kuwa tulikuwa tayari tumefika kwenye kiwanja cha ndenge cha Embakasi. Tulitelemka kwenye ndege. Kisha tulitafuta gari la kukodi twende zetu mjini. Sammy alinunua gazeti la "Sanday Nation" aone kama kuna kitu chochote juu ya tukio hili lakini hakukuwa na lolote, ila mambo mengi juu ya maonyesho ya mavazi na mashindano ya muziki mjini Nairobi. Tulikuwa tumemweleza Chifu asiruhusu hili jambo kuchapishwa mpaka Jumatatu wakati tutakapokuwa tayari tumeanza kazi yetu huko Nairobi.



Tulitazama huko na huko ili tupate gari gani tukodi. Tangu tutoke kwenye ndenge ulikuwa umepita muda wa robo saa na ushee hivi. Nia ya kungojangoja hapo kiwanjani ni kutaka kuona kama kuna watu wowote ambao walikuwa wanategemea kurejea kwetu, kwani siye kushuku kila mtu ndiyo kawaida yetu.



Tulipoona hakuna lolote, tulikodi gari moja la"Archers Tours." Tukamweleza dereva atupeleke mpaka Embassy Hoteli, ambako nduko tulitegemea kulala. Lakini Sammy hakuonelea vizuri wote kukaa katika Hoteli moja kwa hiyo yeye alitaka tumtelemshe Hoteli Pigalle. Tulipanga tuonane mara moja Hoteli Fransae, kusudi tupate kuonana na John Mullunga, kama ilivyopangwa.



Mimi nilishuka Embassy Hoteli, nikaenda katika ofisi yao, ambako nilijiandikisha kama Joe Masanja. Halafu huyo binti ambaye ndiye karani hapo Hotelini akanipa cheti changu, funguo na nambari za chumba. Nikaingia chumbani. Kilikuwa chumba kizuri maana kilikuwa kwenye pembe ya nyumba. Kilikuwa na madirisha mawili. Dirisha moja kwenye upande wa mtaa wa Koinange na moja lilikuwa limezibwazibwa na nyumba zingine. Baada ya kuweka vitu vyangu nilitelemka mara moja kwenda zangu Hotelini Fransae. Nilipopita pale ofisini, nikamweleza mshughulikaji wa simu kuwa kukija simu yangu achukue hiyo habari. Halafu nikampa shilingi ishirini. Akanitazama kwa macho ya kusema asante mara mia. Kwani tarehe ishirini kwenye jiji kama Nairobi, ni mwambo mbaya sana.



Kisha nikaharakisha kwenda zangu Fransae. Nilipofika mlangoni, nilimuona Sammy naye anamaliza kuingia. Nilimuona John amekaa kwenye pembe ya mlango upande wa kushoto kama ukiwa unaingia tu hotelini. Sammy alikuwa hamjui John, kwa hiyo yeye alikuwa bado anaendelea kwenye kaunta ya hoteli. Nilipoingia nilimpigia mluzi akageuka tukamfuata John pale pembeni. Tumewahi kufanya kazi na John huko Kampala, wakati tulipotumwa kuwatafuta waibaji almasi. Na ninakwambia wewe msomaji John kusema kweli si mchezo. Katika kila kesi wanayomweka John hawa watu wa Uganda jua kuna makubwa. John alikuwa amekaa na kijana mwingine mwenye sura ya kupendeza sana. Nafikiri John alimfanya rafiki yake kusudi huyo kijana awe anamtengenezea mpango kwa ndasa, kwani alidhani kuna msichana yeyote ambaye asingesimama kama huyo rafiki wa John akimpigia mluzi.



Tulipofika hapo John alitukaribisha tukae. Kisha akatufahamisha kwa rafiki yake ambaye anaitwa Robin Mwangi, Kikazi akiwa ofisa wa usalama nchini Kenya. Nayo Serikali ya Kenya ilikuwa imemleta Robin kwenye kazi hii. Mimi nilijifahamisha kama Joe Masanja, na Sammy kama Athumani Hassani. Na mikamfahamisha John kwa Sammy kama Fred Kamau. John tayari alikuwa amepata habari zote za kuja kwetu, na jinsi ambavyo Chifu alivyomweleza kama angeweza kumtambua Sammy, kwa kule kuwa na kamera shingoni. Wote tayari tulikuwa tumeshaelezana majina ambayo tutatumia. John alituagizia vinywaji. Aliagizia "Marteli Cognac" toti nane, pamoja na soda kwenye barafu.



Wakati tukinywa, John alitueleza, "Hapa tulipo si mahali pazuri sana kwa kuelezana habari, kwa maana watu wengi huwa wanakuja kuzimua hapa hotelini saa kama hizi, siku za Jumapili. Hata hivyo nitawatolea muhtasari wa habari niliyokwishapata," Alinyamaza, kisha akaanza kusema, "Joe kusema kweli tukio hili linatisha kuzidi matukio yote, kwani inaonekana wote tuko gizani kabisa. Miye nilidhani nitapata jambo lolote la maana lakini wapi. Robin nilimweleza mnamo saa moja aweke vijana wake mahali fulani kusudi huenda wakaweza kutupatia maelezo yoyote ama kama wanaweza kupata fununu yoyote. Lakini ajabu ni kwamba vijana wanne wameisha uawa katika muda huu wa saa mbili. Hii inaonyesha tutakuwa na muda mgumu sana, tena sana.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Mmoja alikuwa amepigwa risasi huko Embakasi. Mwingine ametiwa kisu huko "Uhuru Park". Wengine wawili walikutwa wameuawa huko Lavington Green kwa risasi. Sasa hata hatuwezi kuunganisha vifo hivi, ila tu kwamba watu hawa wako kila mahali. Na linaonekana kuwa kundi kubwa sana. Lakini jambo kubwa ni kwamba lazima tufanye kichwa cha tukio hilo.



"Mkurugenzi wa Idara ya Upelelezi wa kwenu amenieleza kwa simu anavofikiria. Nami ninakubaliana naye, kwani huyu mzee akibashiri kitu, naamini ni hivyo. Kwa hiyo sisi itatubidi tuendelee kama alivyofikiri, la sivyo tumekwisha".



Bado mimi nilikuwa sijaweza kuunganisha jambo lolote. Ilikuwa bado ajabu. Ajabu kubwa. Hapo nilimwuliza John, "Unafikiri, sasa tutaanzia wapi?"



"Mimi nafikiri tutaonana usiku huko Starlight Klabu maana, yule kijana aliyekutwa Uhuru Park, alikuwa sehemu hizo. Na miye nilipochunguza sana ilionekana kama kwamba huyu mtu aliuawa katika nyumba fulani halafu akatupwa Uhuru Park. Kama unavyojua leo ni Jumapili watu wengi walikuwa bado wamelala.



Baada ya kukaguakagua afisa mmoja wa polisi alisema aliona tone la damu kwenye mlango wa Klabu hiyo. Nikaonelea vizuri nimwambie Mkurugenzi wa Usalama wa hapa amueleze Mkuu wa Polisi. Niliwataka wasiulize jambo lolote, au wasiulize maswali yoyote juu ya vifo hivyo mpaka baadaye. Kwa hiyo sasa tutatawanyika halafu tutaonana usiku huko Klabu. Wakati huu Robin na mimi tutaendelea kukusanya habari chache chache toka kwa maafisa wake. Nendeni mkapumzike.



Tuliagana na Robin akanieleza, "Kama ukitaka msaada wowote wa watu waweza kupiga ripoti ofisini kwetu, Chifu huko Dar es Salaam tayari amefanya kila mpango na wakubwa wa usalama katika nchi zote tatu za Afrika ya Mashariki."



Tulikubaliana kuwa wote tutaonana Starlight Klabu mnamo saa tatu usiku. Sammy alienda hotelini kwake, nami nikarudi hotelini kwangu kupumzika kidogo.



Nilipoingia hotelini kwangu nikaenda mpaka kwa mshughulikaji na simu kumwuliza kama amepata simu yoyote. Naye akasema kwamba alikuwa bado hajapata. Nilienda moja kwa moja kitandani kwangu nikalale.



Nilipoamka ilikuwa saa kumi na mbili za jioni. Nilioga na kunyoa ndevu. Halafu nikajitayarisha kwa kila njia ili niweze kuonekana kama mwandishi kweli kweli. Halafu nikaagiza chakula. Sikula chakula kizito sababu hali yangu haikuwa nzuri sana. Baada ya kula nilimpigia simu Sammy anipitie mnamo saa mbili na nusu.



Ilipofika saa mbili na nusu Sammy alinikuta baa ya Fransae. Tukafunga safari kwenda Starlight. Mimi nilitaka tuchukue taxi, lakini Sammy alikataa, kwa kusema, "Twende kwa mguu, maana tunaweza tukapata jambo la kufurahisha. Pia ni lazima uchukue bastola yako, maana kunaweza kuwa na mambo ya hatari."



Nilirudi chumbani kwangu, nikaweka bastola yangu ndani ya mkoba wake wa begani. Nikaweka koti langu juu nikafunga tai sababu mwezi wa saba, ni baridi sana Nairobi. Ningekuwa sehemu za Dar es salaam, wakati huo ningekuwa ninavaa furana. Kweli nilipojiona kwenye kioo nilionekana mwungwana. Na ninakwambia ninapokuwa nimevaa koti, huwezi kujua kuwa hata siku moja nimewahi kugusa bunduki. Nilirudi huko, baa kumpitia Sammy ili twende zetu.



Tulienda na mtaa wa Koinange, halafu tulipofika New Avenue Hoteli, tukashika Kenyatta Avenue. Tuliendelea na Kenyatta Avenue mpaka tuliposhika Uhuru Highway, tulikoingia katika kijinjia kinachopitia Uhuru Park. Tuliangaza huku na huko katika Uhuru Park lakini ilionekana hapakuwa na watu. Nadhani watu walikuwa wameishasikia kifo cha huyo kijana. Pia tulitegemea kuwa kama watu hao wamekuwa wakifuata myenendo yetu, huenda wakawa wanatufuata. Hivyo Sammy akawa tayari tayari na visu vyake ikiwa kutatokea matata. Lakini hatukupata jambo lolote.



Tulipoachana na Uhuru Park, tulishika Kirk Road. Tukaenda zetu moja kwa moja mpaka Starlight. Nje ya Klabu hiyo tulikuta watu wengi wakikata tikiti. Wanawake walikuwa wengi sana hapo nje, na walionekana wakitafuta wanaume wa kuwaingiza ndani. Lakini sisi tulikata shauri tusiwajali maana wangeweza kuingilia kazi yetu. Nilienda nikakata tikiti halafu tukaingia ndani.



Hii Starlight Klabu inapendeza mno maana hali ya hewa ya humo ndani ni tulivu kabisa. Kila mtu alionekana ni Mwungwana. Watu wengi walikuwa wameishaingia. Wengi wao walikuwa wawili wawili, yaani" Kitu Mtu." Nadhani unanielewa ninaposema hivyo. Tulienda tukakaa kwenye pembe moja ya kulia karibu na mlango mkubwa wa kuingilia. John alikuwa bado hajafika. Tulishangaa sana, lakini tulijua tu ya kwamba atafika muda si mrefu. Punde si punde Robin alifika. Na mara alipotuona akatufuata.



Robin aliuliza, "Fred yuko wapi?"



"Hata siye bado hatujamuona. Tulidhani mngefika wote hapa, "alijibu.



"Hata, aliniambia kuwa yeye atakuwa hapa mnamo saa mbili u nusu, kama ni hivyo basi huenda yuko kwenye ile baa ya nje, au amepata habari fulani ambayo anaishughulikia."



Kisha Robin aliondoka akaenda kwenye baa ya nje kuchunguza kama Fred yuko huko. Aliporudi alitueleza kwamba Fred hakuweko. Sammy aliagiza vinywaji. Muziki nao ulianza kupigwa na vijana wa Fiesta Matata ambao hupiga muziki taratibu kabisa. Wakati huo wote tulikuwa tukimngojea Fred lakini hakuonekana. Tulianza kupatwa na wasiwasi mwingi sana. "Kwani Fred anaishi wapi?" Sammy alimwuliza Robin.



"Anaishi Princess Hoteli."



"Afadhali nikampigie simu huenda anaumwa," nilisema



"Sammy uwe unaangalia kama yuko mtu mwenye shauku na mimi nipigapo simu."



Nilipopiga simu hotelini kwa Fred ilionekana hayuko kwani kengele iliendelea kulia kwa muda mrefu sana. Nilikata simu na kurudi pale kwa akina Sammy. Niliporudi Sammy alinieleza, "Ulipokuwa ukienda msichana mmoja ambaye alikuwa amevaa mini alikuwa akikuangalia kwa jicho la pembeni pembeni. Msichana huyo alikuwa akicheza dansi na kijana fulani. Halafu alipokuona ukienda kwenye simu alisogea mpaka kwenye kiti cha karibu na simu, kisha akajifanya kuwa anasoma gazeti. Na baadaye msichana huyo akapotea mumu humu mwenye watu."



Hilo jambo niliona huenda ni hatua moja wapo. Lakini hatua hii ilikuwa bado haina uhusiano wowote na tukio letu. huenda ni kwa sababu ameona ajabu kwa nini tulipiga simu, na kwamba tulikuwa tumekaa tu bila wanawake na hali tunaonekana vijana nadhifu mno.



"Habari zenu," sauti nyororo ilitoka kwa nyuma yetu. Kila mtu kati yetu alipatwa na kigugumizi cha kujibu, kwani wote tulipotupa macho nyuma yetu, tulimwona msichana mzuri mmno!



Nakwambia maishani mwangu nimeona wasichana, lakini ilivyo ni kuwa huyu msichana alishinda. Nilisikia nywele zikinisimama nilipomwangalia tena. Nilijikaza kisabuni nikamjibu, "Siye wazima tu, vipi wewe?"

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Miye salama tu. Nilidhani kuwa huenda nyiye ni wageni hapa. Na kwamba huenda mlipofika hapa mlifanya mpango na wasichana fulani fulani mwonane nao, lakini hawajaonekana, si hivyo?"



"Kidogo huenda uko sawa, lakini si sana,"nilimjibu.



"Mbona unaonekana mwenye wasiwasi basi? Nilidhani kwamba ulienda kupiga simu kwa madhumuni ya hao wasichana." Akanyamaza hali akinitazama machoni.



Kweli mimi nakwambia sitaki wasichana wanaonitazama machoni. Kwa hivyo msichana huyu mara moja alinitisha. Macho yake yalionekana kusinziasinzia, lakini yanaweza kukusoma moyoni mwako.



"Nilikuwa napiga simu kwa rafiki yangu mmoja ambaye ni mwandishi juu ya mambo ya muziki. Yeye tulimwacha Acadia Klabu. Nilitaka kumweleza aje huku kwani, muziki wa hapa unaonyesha umeshinda. Lakini inaonekana kuwa muziki wa huko umewaingia sana hata hawasikii mlio wa simu," niliongopa.



Alitabasamu. Tabasamu hilo lilifanya nywele zangu zisimame tena.



"Kweli nimeupenda muziki wa hapa," alisema msichana huyo. "Hata mimi huwa napenda bendi hii hii, na mahali papa hapa."



"Jina lako nani, "aliulizwa na Sammy.



"Mimi naitwa Lulu. Lulu Jack, kazi yangu ni kuonyesha mavazi. Nimetoka Kampala kuja kwenye maonyesho ya mavazi hapa Nairobi ambayo yatachukua kama wiki mbili hivi." Alinyamaza kwa muda wa kupisha mate yapite kooni. Kisha akauliza," Na nyiye ni akina nani?"



"Miye ni Athumani Hassani, na huyu," alisema Sammy akionyesha kidole kwangu," ni Joe Masanja. Na huyo ni Robin Mwangi. Kazi yetu sisi ni uandishi wa habari juu ya maonyesho ya mavazi. Hata sisi tumeletwa na yaya haya maonyesho ya mavazi. Hivyo inaonyesha tutaonana mara nyingi toka sasa. Naamini nitakuwa mtu mwenye furaha sana nitakapokuwa nakuchukua picha. Maana mimi ndiye mchukuaji picha katika kundi letu hili."



"Nitafurahi sana kuzidi kuonana na nyinyi kwani mnaonekana kuwa watu waungwana sana. je, mnatoka wapi?" Aliuliza.



"Siye tunatoka mjini Mwanza, Tanzania," alijibu Sammy. Kisha Lulu alituaga akaondoka kwenda kucheza dansi. Mimi huwa siwaamini wasichana wazuri kama hawa. Nakumbuka siku moja mama yangu, Mama-Willy, alinieleza kuwa kati ya wanawake wote, ukiona mwanamke mzuri sana jua mwanamke kama huyo ni hatari sana. Na nilipoanza kazi kila siku ninapotumwa kwenye shughuli fulani jambo la kwanza la Chifu ni kunisihi nisifuate wanawake wazuri sana. Maana wanawake kama hao ni sumu kali sana. Lakini mimi Willy, ingawaje nakubaliana na Mama Willy pamoja na Chifu, nimekuja kutambua kutokana na kazi zangu kuwa, kutokana na mwanamke mzuri sana unaweza kupata habari za ajabu sana. Nilikata shauri kuwa sitamwachia Lulu vivi hivi lazima nitafute mengi ya maisha yake.



Huyo mtoto Lulu ni Lulu kweli kweli. Kwani toka kwenye dole gumba mpaka utosini hana dosari yoyote. Ukimwona hutaamini kuwa alizaliwa na mwanadamu ila labda mtoto wa jini, kama unaamini kuwa kuna majini, ama amefyatuliwa kutoka katika mashine baada ya kuchongwa na mchongaji nambari moja hapa ulimwenguni. Nakwambia kama Lulu ataacha wazi sehemu ya kifua chake halafu umtazame, utababaika. Hutaweza kumwangalia mwanamke mwingine yeyote. Utawahesabu wanawake wengine kama wanaume tu. Kama Mungu amewahi kupendelea, basi huyu Lulu amempendelea hasa.



"Sammy," niliita, "angalia kila mtu anayehusiana na Lulu katika hii klabu. Nawe Robin pata watu wa kumfuatia Lulu ili tupate kujua anakaa wapi." Nilinyamaza kidogo kisha nikaendelea, "Mimi itanibidi niende kule hotelini kwa Fred nikajue kuna nini, maana mpaka sasa yapata saa nne na nusu na bado hajaonekana. Ninawaacheni wote hapa ili kuangalia mambo ya hapa klabu. Lakini Sammy unipigie simu kama ukiona nimechukua muda mrefu, zaidi ya dakika arobaini na tano. Na upige kule kule chumbani kwa John. Kwaherini." Nikaondoka.



Nilikodisha gari nje na kwenda moja kwa moja mpaka Ambassador Hoteli. Sikutaka anitelemshe hapo Princess Hoteli. Niliposhuka hapo, ilinibidi nichukue Government Road nionekane kama kwamba nataka kuchukua 'bus' kwenye kituo cha 'mabus' cha Ambassador. Nilikwenda nikazungukia mtaa wa Duke, halafu nikaingia katika mtaa wa Tom Mboya.



Nilipoingia Princess nikakuta watu wengi sana katika baa. Nikajifanya kama miye pia mpangaji wa hapo lakini nilitazama huku na huko hapo hotelini ili nione kama kuna mtu ananichunguza. Lakini watu wote walionekana wakishughulika na unywaji wa pombe na kadhalika. Nilipanda ngazi mpaka ghorofa ya kwanza, Robin alikuwa amenipa nambari za chumba ambamo John alikuwa akilala. Nilikwenda mpaka kwenye hicho chumba. Kabla sijagonga nilikagua vyumba viwili vilivyokuwa upande wa kuume na kushoto wa hicho chumba. Lakini sikuona wa kusikia chochote. Ilionekana hivyo vyumba havikuwa na watu, au wote walikuwa wamekwenda kutembea.



Niligonga kwenye mlango wa John lakini sikusikia lolote. Nikafikiria kutoka, lakini nikaona afadhali niingie ndani pengine nitaweza kupata habari zozote. Ama huenda akawa ameacha habari fulani fulani. Nilichukua funguo zangu malaya ili nifungue mlango kwani ulikuwa umefungwa.



Nakwambia sijawahi kushituka kama nilivyoshitushwa na hali niliyoikuta humo chumbani nilipowasha taa. Hofu iliniingia, nikaanza kugwaya. John alikuwa amelala kifudifudi. Amekufa! Fahamu zilinitoka kwa muda wa dakika tano hivi. Baada ya kuzinduka nikaenda karibu na maiti ya John ili niichunguze vizuri. Niliona kuwa alikuwa amepigwa risasi sita, zote kifuani.



Ilionekana kuwa huyo aliyempiga hizo risasi, bastola yake ilikuwa .45. Kwani miye nimewahi kuona matundu ya risasi hizi. Haya mauaji yalikuwa ya kutisha sana. Yalikuwa mauaji ya kikatili sana, maana aliyemwua alimwachia risasi nyingi kana kwamba alimwua ng'ombe. Na ilionekana kwamba waliingia kwa ghafla, kiasi ambacho hata John hakuweza kujitetea.



Kifo hicho cha John kiliniuma sana hata nikaapa kuwa huyo aliyemwua, lazima nimkamate na kumwua mimi mwenyewe, kama nitakuwa mzima wakati wote wa madhila kama hayo. Woga ulianza kuniingia kwa mara ya kwanza.Tangu nianze kazi hii sijapatwa na woga kama huo. Kitu kilichofanya nitishike sana ni jinsi wauaji hao walivyomfahamu John. Na kama ni hivyo, basi hata sisi tutakuwa tumeisha fahamika. Na kama wameweza kumwua John ambaye ni mpelelezi mashuhuri katika Afrika ya Mashariki, lazima watu hawa wawe miamba kweli. Na lazima wawe ni wenye akili nyingi sana juu ya kuwinda watu.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Kweli tulikuwa tunanuka vifo siye sote. Hazijapita hata saa ishirini na nne, watu watano tayari wameishakufa! Hata kama ungekuwa na moyo mgumu kama wa Farao, hata wewe ungeweza kutishika.



Nilikata shauri, kuufunga mlango na kuiacha hiyo maiti halafu niende kuwapigia simu polisi. Lakini kabla sijatoka niliona heri nipekuepekue mifuko ya John ili huenda nikapata kitu chochote kilichofanya hata wamfuate. Na kama unafikiri sana unaweza kuona kuwa lazima John, wakati sisi tunashangaashangaa yeye alikuwa amegundua jambo fulani ambalo ndilo lililosababisha kifo chake. Kisha nilienda mpaka kitandani ambako kulikuwa na mkoba. Nilipoinama tu,nikasiki sauti ikiniambia,"Tafadhali kaa ulivyo wala usisogee hata inchi moja. La sivyo utapata idadi ya risasi zile zile zilizomwingia huyo mshenzi karibu nawe hapo."

Nikaduwaa....!





Nilijiona siwezi kufanya lolote. Na kama kweli ningefanya upuzi hapo, nilijua hata mimi ningeyala marisasi. Kwa hiyo nilionelea ninyamaze tu mpaka hapo nitakapopatiwa yangu. Jinsi huyu mtu alivyoingia hata sifahamu maana aliingia kama mchawi bila hata kishindo. Zaidi nilikuwa nataka nimwone ni nani, lakini niliona kwamba ningegeuka uso tu, ningekwisha kazi. Nilijua hata mimi huo ndio mwisho wangu. Mara nyingi huwa katika hatari kama hizi, lakini kwa mwujiza wa Mungu hutokea nikaponyoka. Mara hii mambo yalionekana kuwa tofauti kwani watu hao hawakuweza kufanya kosa hata moja.



"Wewe ni nani, na unafanya nini hapa?" Niliulizwa.



"Mimi naitwa Joe Masanja, na nimekuja hapa kumtazama huyu Fred Kamau ambaye ni mwandishi mwenzangu. Sote tunaandika habari juu ya maonyesho ya mavazi ambayo yameanza hapa. Na nimestaajabu sana kumkuta ameuawa." Nilinyamaza kisha nikasema kwa upole mwingi, "Lakini mbona unanijia kijeshi namna hii, kama kwamba miye nimefanya jambo lolote? Ninashangaa kujiona nimeshikiliwa bunduki mgongoni. Ninaweza kuzimia hivi. Na wewe ni nani? Niliuliza.



"Nyamaza," alijibu "sina muda wa kujibu maswali yako, nimo kazini. Ila nataka kujua uliingiaje humu! Mlango ulikuwa umefungwa. Na kwa nini baada ya kuingia humu ukaonekana kuchunguzachunguza vyumba vilivyo karibu na hiki, kama kwamba ulikuwa ukijua kwamba ulikuwa unafuatwa?"



"Nilifungua mlango kwa kutumia ufunguo niliopewa na huyu rafiki yangu Fred, maana alikuwa na funguo mbili. Nilikuwa nimesahau nambari ya chumba ndiyo sababu ilinibidi nithibitishe ni kipi kati ya hivi vitatu,"nilimjibu. Wakati huo zilikuwa zimepita dakika arobaini na saba, na simu ilikuwa bado haijalia. Hivyo nilizidi kukabiliwa na wasiwasi.



"Wewe ni mwongo - mwongo nambari moja. Hii inaonyesha unafahamu mambo mengi kuliko hivyo unavyotaka kusema. Huyu si Fred ila ni afisa wa upelelezi aitwaye John Mullunga," alijibu kwa sauti ya hasira. "Na siye tulikuwa tunajua kwamba atakuja mtu wa aina yake kuangalia. Na wewe lazima ni mmoja wao, ila tu unajidai ni mwandishi. Hivyo lazima na wewe ufe kusudi tuweze kuendelea na mipango yetu."



"Hayo ni maneno yako wala si yangu. Na hata kama ukiniua, siku moja nawe utakamatwa. Miye sikuwa nikijua kuwa huyo ndiye John Mullunga. Na wewe tu ndiye umeniambia maneno haya. Na kama huyu kweli ndiye John Mullunga ambaye nimesikia habari zake, na nyiye mmemwua, basi serikali ikifahamu, itawawinda mpaka watawatia vitanzi." Nilimueleza.



Wakati wote huu nilikuwa nasema kusudi dakika zizidi kwenda ili pengine baadaye nipate mkombozi. Alianza tena kunitisha, "Maiti huwa hazielezi habari. Sitakusikiliza kwa maana wewe ni maiti tayari." Alianza kucheka kisha akaniambia,"Toa sala zako za mwisho. Na kama wewe pia ni afisa wa upelelezi, serikali itatukoma, maana hizi serikali bado hazitutambui. Na 'bosi' wangu nadhani atafurahi sana kusikia John amekufa na kijishenzi kingine."



Wakati huu wote nilikuwa nafikiri namna ya kuweza kujiponyesha. Lakini niliona hakuna. Bastola yangu nilikuwa nayo kwapani lakini nilijua nikijitingisha kidogo tu nitaingia kuzimu! Kwa hasira na uchungu nikasema, "Niue basi sasa unafanya nini? Unapoteza muda wako."



"Fumba macho, usali kwa dini yako, ama vyovyote."



"Naomba nipige magoti basi." nilisema.



Alicheka akasema, "Lo! Nadhani polisi watakaokuja humu watapata tishio, kwani watakukuta wewe umekula risasi sita hali umepiga magoti kitandani unasali. Halafu wataona rafiki yako amelala kifudifudi hapo chini, akiwa kama anaomba msamaha. Naye pia amekula risasi zipatazo sita." Sauti ya huyu mtu ilinionyesha kuwa ni mwuaji, na ni mtu ambaye anafurahia kuua. Pia alionyesha kuwa mtu katili na jambazi.



Nilikuwa wakati wote huu nikifikiria njia ya kujiokoa. Na kule kuomba nipige magoti, ni jaribu la kwanza kama huyo mtu akikubali tu nimtengeneze mara moja. Nikajifanya kuwa nilikuwa natetemeka ovyo. Bastola yake ilikuwa nusu inchi kutoka kwenye mgongo wangu. Nikabaki katika kufikiria jinsi ya kuirusha. Nilijua kuwa mtu huyo alikuwa mwuaji na hatanihurumia.



Mama-Willy alinishauri siku moja kwa kusema. "Mwanangu kama umo hatarini, usife kama kondoo, kufa kama mwanaume ambaye wakati wa kuzaliwa mama yake alishikwa na uchungu wa ajabu."



Tangu siku hiyo sikukubali kufa kikondoo. Basi niliposogea kwenye kitanda, hili jambazi lilipitisha mkono kwenye koti langu. Likatafutatafuta na kukuta bastola yangu ambayo aliichukua. Halafu likacheka. "Yee, eti wewe ni mwandishi. Mwandishi gani anatembea na bastola, automatic '45' katika Afrika ya Mashariki? Mawili, wewe ni jambazi ama afisa wa upelelezi."



Wakati huo akizungumza nilijua nimeishapatikana. Nukta yoyote ningeweza kula risasi. Na kicheko alichocheka kilikuwa cha hasira. Nilisikia akiitupa bastola yangu upande mwingine wa chumba. "Upesi piga magoti. Huwezi kunidanganya mimi ati ni mwandishi. Ingekuwa Marekani ningelikubali, lakini Afrika ya Mashariki usinitanie."



Wakati ninapiga magoti na huku najifanya kama kwamba natetemeka, nilitupa shoto langu kama umeme. Kufumba na kufumbua, bastola ya hilo jambazi iliruka na kwenda kwenye pembe moja ya chumba. Hapo hapo nikamgeukia. Akanitupia ngumi moja, nikaikwepa. Nikatupa shoto langu tena likampata kwenye taya mpaka chini. Ilivyo ni kwamba shoto langu likikupata, ukiwa dhaifu hutaamka tena hadi siku Yesu atakapokuja kwa mara ya pili!



Niliruka mpaka alipo, lakini akanipiga kwa mguu tumboni. Nikaenda kuangukia kitanda! Wakati huo alikuwa ameisha simama. Akanijia wakati nikijaribu kusimama. Akanitia ngumi shingoni na kujikuta niko chini! Halafu akanitia teke la usoni na kuikimbilia hiyo bastola. Kabla hajafika niliruka kama swala na kumchukua 'judo' mpaka kitandani. Katika maisha yangu ya miaka sita katika kazi hii sijaonana na mtu kama huyu. Kweli siku hii, lo, maisha yaliniwia magumu.



Kabla hajasimama nikamtia ngumi nyingine kwa mkono wangu wa kulia. Na hapo nikaona amedhoofika. nikaondoka kukimbilia bastola. Kabla sijafika nilipata teke la mgongoni na kunifanya nipepesuke. Kabla hajashika hiyo bastola nilimpa tena shoto langu mpaka akaanguka chini. Nilimfuata hapo chini na kumtia teke la tumboni, na jingine ubavuni. Maana majitu kama haya, ukijigamba kuyapiga kichwani tu utacheka. Yanavyo vichwa vigumu kama paka.



Alipodhoofika kabisa niliiendea bastola. Kurudi nikakuta amezimia. Ilikuwa yapata saa tano na robo za usiku sasa. Niliendea chupa ya "whisky" iliyokuwa humu chumbani na kuanza kummwagia na kumnywesha kidogo kidogo. Kisha akaanza kuzindukana. Hapo nikashikilia bastola yangu kwenye taya lake.



"Niambie wewe ni nani, la sivyo utameza risasi zote hizi zilizomo katika hii bastola," nilimwambia.



"Yeeeh, sitaweza kusema hata ufanye nini na afadhali uniue tu," alijibu.



"Sasa kama hutaki kusema jina lako huyu uliyemuita 'bosi' wako ni nani?"



Hakujibu alinyamaza tu. Nikaona nisipokuwa katili hapo sitaweza kupata fununu yoyote. Niliwasha kiberiti changu. "Usiponieleza jina lako nitakuchoma masikio yako ingawa unaonekana kuwa hujali."



Basi nilisogeza moto kwenye sikio lake nikaanza kumchoma. Kwanza alijifanya hajali ingawaje alionyesha kuhisi uchungu wa ajabu. Hii ilinionyesha kuwa yeyote yule ambaye anaitwa 'bosi' wa watu hawa lazima anajua kuchagua watu wake. Kwani kweli ni wanaume. Ni watu wachache sana wanaoweza kuvumilia moto. Lakini maumivu yalipozidi alianza kuguna halafu akaanza kulia.



Mwishowe alisema, "Acha, niachie, nihurumie. Ngoja nitakwambia, hebu niache."



Nilitoa moto penye sikio lake kumpa nafasi aseme.



"Mimi naitwahttp://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Kabla hajasema jina lake alipigwa risasi toka dirishani. Akafa! Niligeuka kutazama aliyemwua, lakini sikuona mtu. Na wala sauti ya bastola au bunduki iliyomwua sikuisikia. Hii ilionyesha kuwa bastola zao zote zina viwambo vya kunyamazisha sauti, ambavyo huitwa "sailensa."



ITAENDELEA 

0 comments:

Post a Comment

Blog