Search This Blog

Friday 18 November 2022

KUFA NA KUPONA - 2

 






Simulizi : Kufa Na Kupona 
Sehemu Ya Pili (2)




Kupigwa risasi kwa mtu huyo kulinipa wasiwasi zaidi. Moyo ulipiga mara nyingi mno. Chuki ilinijia maana hawa watu wanaonekana kuwa wameipanga mipango yao kiasi cha kwamba wanahakikisha hawafanyi makosa, hata chembe ya kosa. Nilikata shauri nitoke hapo mahali. Niliangalia zile maiti kwa mara ya mwisho. Nikaamua kwenda kuuchunguza ule mfuko wa John kabla sijaondoka. Lakini kabla sijafika kwenye huo mfuko, nilisikia sauti ikisema, "Simama hapo hapo ulipo, na usijitingishe."



Moyo uliniuma na hofu ilinizidi kwani niliona mara hii hawatafanya makosa kama mara ile.



"Angusha chini bastola yako," mtu huyo nisiyemtambua alisema kwa sauti ya hasira.



"Geuka unitazame."



Niligeuka upande wake na huku nimeinua mikono juu. Huyo mtu alionekana katili zaidi ya yule mwingine. Alikuwa kijana mwenye sura mbaya mbaya. Mweusi na mwenye umri upatao miaka ishirini na minane. Kwa umri tulikuwa tukilingana.



Mimi pia nilikuwa nina umri wa miaka ishirini na minane. Na kuadhimisha sikukuu yangu ya kuzaliwa ilikuwa wiki moja toka siku hiyo. Nilimwacha Della akialika watu kwenye hiyo sikukuu yangu. Lakini huenda badala ya kuadhimisha sikukuu yangu ya kuzaliwa, watakuwa wakiadhimisha matanga yangu, siku hiyo. Maana sasa kila dakika ilinuka kifo kitupu.



"Mara hii hatutafanya makosa. Huyo mshenzi waahedi hapo chini, alifanya makosa na ndiyo sababu na yeye amepata zawadi yake. Wewe ni nani? Maana unaonekana kuwa tisho kwetu zaidi ya wengine wote. Hakuna aliyewahi kupambana na Kasha akabaki mzima. Hebu nipe maelezo kwa kifupi. Maana utake usitake utakufa tu. Huwa sifanyi makosa mimi."



Nilipomtazama alionekana kuwa mtu ambaye hawezi kufanya makosa. Niliomba Mungu kimoyomoyo na kuanza kutubu makosa yangu.



"Mimi naitwa Joe Masanja. Na ni mwandishi wa habari juu ya 'Maonyesho ya Mavazi," Nimetoka Mwanza. Tanzania," nilisema.



"Pumbavu wee, unadhani unaweza kunidanganya mimi, mwandishi hawezi kuwa jasiri kama wewe hata kuweza kumshinda nguvu Kasha," alisema, kisha akanipiga kofi moja mpaka nikaona jua, ingawaje ilikuwa usiku. Fahamu zikaniruka kwa muda. Ziliporudi nilikuta bado ameshikilia bastola yake na kuniuliza tena mimi nilikuwa nani. Nilimjibu vile vile, "Oke, oke, mimi sitajali kama kesho nitakuona ukila chakula cha mchwa," alisema kwa kiburi sana.



Nilifumba macho maana niliona ndio mwisho wa maisha yangu. Hapo sikuwa na ujanja wowote . Kwani huyu kijana anavyoshikilia bastola, afadhali naye yule, mchezaji wa sinema wa kule Mexico, "Cowboy Cuchilo."



Wakati nilipoona anakaza mkono wake kuachia risasi, kufumba na kufumbua nilishtukia anaanguka chini. Alikuwa amepigwa risasi! Taratibu akakata roho! Niliruka mara moja kuchukua bastola yangu tayari kwa matata mengine yoyote. Mlango ulipofunguliwa nilikuta ni Sammy.



Kwa mara nyingine tena Sammy alikuwa ameponyesha maisha yangu, la sivyo dakika hii ningekuwa mfu.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Willy - naona walikuwa wamekusakama sana. Sasa, tukimbie tutoke hapa ili ukanieleze jinsi mambo yalivyokuwa, alininong'oneza Sammy.



Kulikuwa na maiti tatu hapo chumbani sasa. Kabla sijatoka hapo chumbani nilienda kwenye mkoba na kuanza kukagua kagua. Nikaona hamna la kutusaidia. Tulipitia dirishani na kutelemkia kwenye ukuta na kutokea kwenye kijinjia.

Tulikimbia toka hapo mpaka River Road.



"Nilipiga simu baada ya dakika arobaini na tano kama ulivyosema," alisema Sammy," Simu ilionekana kuwa ilikuwa imekatwa, kwa hiyo tukaanza kuingiwa na wasiwasi. Ikabidi tungojee kwa muda wa dakika ishirini tena. Nilipotoka tu baada ya dakika kama tano hivi Lulu naye hakuonekana tena. Pia vijana fulani watatu waliokuwa wakienda lakini tukaona mambo yasingekuwa mazuri sana kwako. Maana usingalijua tumekwenda wapi. Baada ya kungoja kwa dakika ishirini tena, mimi na Robin tulianza kuwa na wasiwasi. Kwa hiyo mimi nikakata shauri nikufuate na kumwacha Robin humo Klabuni kuzidi kuchunguza.



Nilichukua taxi hapo nje mpaka nyuma ya Hilton Hoteli na kuanza kutembea kwa mguu mpaka hapa hotelini. Ndani ya bar watu walionekana kushughulika na ulevi. Kwa hiyo mimi nilienda kwenye kaunta na kuagiza 'bia' moja. Nilianza kumwangalia kila mtu kwa usiri sana. Mwishowe ndipo nikamwona mtu akipenya kwa haraka kati ya mlango mmoja unaotokea nje kwenda mwenye vyumba vya kulala. Huo mlango umeandikwa "HAKUNA KUPITA HAPA."



Nilipoona hivyo nilitoka kwenye 'kaunta' kwa siri na kuingia katika vyumba vya huko juu. Halafu nikangoja. Kwanza mtu huyo aliingia katika chumba cha mkono wa kulia. Baada ya kukaa kidogo alitoka na kuingia humu. Wakati wote huu miye nilikuwa nashindwa kutoka, kwani kulikuwa na wafanyakazi wa humu hotelini wakifanya kazi.



Alipotoka ndipo nikakimbia na kuingia katika chumba cha upande wa kulia. Baada ya kuchungua sana niliona hakikuwemo chochote humo. Ila ukutani katika pembe moja kuna matundu matatu. Haya matundu yanatosha kuingiza mdomo wa bastola. Na ninadhani ndimo huyu mtu wa pili alimomwulia mtu wa kwanza. Na kwa kutumia tundu hilo hilo ndimo mimi nimemwua huyo jamaa. Na nimetumia 'sailensa' hata mimi," alimaliza Sammy.



Na mimi nikamweleza mambo yote yalivyotokea.



Sasa tulijaribu kuunganisha mambo yote yalivyotokea.



Inaonekana hawa watu walijua John amekuja kufanya nini kwa hiyo walitumia kila njia wamwue. Pili wanajua kuwa kuna watu ambao watafanya kazi hii na John, hivyo walikuwa wanavizia mtu yeyote ambaye angekuja katika chumba cha John. Nilipokuwa nimepiga simu mara ya kwanza inawezekana hawa watu walikuwa chumba cha pili. Nilipokata simu, nadhani walionelea wakate waya wa simu, ndiyo sababu wewe uliponipigia haikuweza kulia kengele.



Nilipofika mimi walijua lazima ndiye mwenzake John, hivyo lililokuwepo ni kuniua hata mimi. Nilipoweza kumshinda Kasha. huyu mtu wa pili alikuwa chini ya hoteli akimngojea Kasha. Kasha alipokawia akaona aje aangalie. Alipofika humu hakuja moja kwa moja, akaona aingie mwenye chumba hicho cha pili sababu alijua kuwa wameshatayarisha hayo matundu. Alipochungulia aliona nimeshamshinda nguvu Kasha. Na Kasha alikuwa karibu atoe siri, kwa hiyo ikambidi amwue Kasha kabla hajasema.



"Angeniua na mimi papo hapo lakini alitaka kuwa na hakika mimi ni nani, kwa vile alivyodhani anaweza kunilazimisha kusema. Nilipokataa kumwambia uhakika aliona aniulie mbali, lakini wewe ukamuua kabla. Huyu mtu wa pili alionekana kuwa wa maana zaidi katika huu uhaini kuliko Kasha. Sasa lililopo ni kutaka kujua hawa ni akina nani." Nilinyamaza kumeza mate.



"Maswali ya kujiuliza sasa ni mawili au matatu. Je walimfahamuje John, mapema hivi? Je huyu mwenye hoteli ana uhusiano nao? Sammy alitaka kuzungumza.



"Willy mimi naona kuwa wewe uende tena huko Princess maana sasa ni saa sita kasoro robo. Miye nitarudi Starlight nikamwone Robin. Huenda akawa na jambo. Halafu wewe nenda kazungumze na wafanyakazi wa hapo upate kujua lini chumba hicho kimeacha kutumika. Nadhani vijana wa Robin wamemvia Lulu kwa hiyo huenda Robin anaweza kuwa na jambo juu ya Lulu na watu wake. Hizo maiti hazitatambuliwa huenda mpaka kesho asubuhi. Hii itatupa muda wa kutosha kufanya kazi zetu.



Ukitoka Princess njoo moja kwa moja mpaka Starlight Klabu kabla ya saa saba. Ukichelewa tutajua huenda umesakamwa na siye tutakimbia kuja hapo."



Mawazo ya Sammy niliyaona kuwa ya busara sana. Kwa hiyo tulifanya kama alivyosema. Nilikodisha gari toka River Road kupitia Compos Robeiro mpaka Princess. Sammy naye akakodisha gari kwenda zake Starlight.



Nilipofika Princess nilikuta watu wote bado wanashughulika na kunywa, na kila mtu alijali mambo yake. Wengi walikuwa wakimalizia vinywaji vyao kwani saa za kutoka zilikaribia. Katika pembe moja nilimwona msichana mmoja ambaye hakuonekana mwenye furaha hapo halipoketi. Nilipokuwa nikimfuata hakuonekana kupenda nimfuatie hivyo.



"Habari zako binti," nilimsalimu. Badala ya kunijibu alinitizama tu. Nilikaza roho kiume, nikaenda kukaa kwenye meza moja naye. Uso wake ulionyesha uhasama wa chuki, ingawa sura yake ilikuwa na haiba kiasi cha kutosha .



"Mbona nyiye wanaume hamwezi kujali mambo yenu wenyewe? Huko kuniona hapa unadhani mimi natafuta wanaume?" Alisema kwa dharau.



Si hivyo bibie. Miye mwenzio si mwenyeji sana hapa. Nimekujia ili unisaidie mambo mawili hivi. Na hakika nilistaajabu kuona kisura kama wewe kukaa peke yako hapa pembeni tena ukionekana mwenye kuwa na huzuni. Je, kuna jambo lmekuudhi? Ama ikiwa ni shemeji aliyekuudhi, nitumie nikamsihi," Nilinyamaza nikitabasamu.



"Sema basi unataka nikusaidie nini? Miye hapa napumzika na kawaida yangu huwa sipendelei sana kukaakaa na wanaume wanaokunywa pombe. Ndiyo sababu nimekaa hapa peke yangu. Wewe ni nani?" Aliuliza.



Mimi ni Joe Masanja, mwandishi wa habari juu ya maonyesho ya mavazi. Ninatoka Mwanza. Tanzania. Hii ni mara ya yangu ya kwanza kufika Nairobi. Nina haja ya kujua baa hapa Nairobi zinafungwa saa ngapi siku za jumapili?"



"Nenda uulize huko baa," alijibu kwa hasira.



"Ah binti! Mbona wasichana wa Nairobi wakali hivi? Msichana kama wewe hufai kuwa mkali kwa kijana kama mimi. Uzuri wako unakutaka uwe mkarimu na msikivu ili uweze kuziliwaza nyoyo za watu dhalili kama miye." Nikamjengea tabasamu pana la haiba.



Maneno hayo yalimlainisha kiasi. Ukitaka msichana afurahi, mwambie kuwa midomo yake ni mizuri na mitamu.



"Wanafunga saa saba, lakini unaweza unafungiwa ndani ukaendelea kunywa mpaka huenda hata saa tisa," alijibu.



"Jee unaitwa nani, na unakaa wapi?"



"Mimi naitwa Lina Samson. Kwetu Nakuru, lakini kwa sasa niko hapa kwa mapumziko kidogo ya mwezi mmoja. Ninaitambua vyema Nairobi sababu nilizaliwa nikakua na kusoma papa hapa mpaka baba alipohamia Nakuru, ambako ndiko masikani hasa," alijibu hali akimwemwesa.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Sijui kama nitakuona tena Lina. Ningependa kukuona mara nyingi kama hutajali,"



"Ninaishi Guaden Hoteli chumba nambari kumi. Unaweza kupiga simu hapo hotelini, na watakuunganisha na chumba changu. Alamsiki," alimalizia hali akisimaa kujiandaa kuondoka hapo. Akaondoka.



Nilizunguka zunguka kidogo humo ndani kusudi niweze kuona kama naweza kumpata mfanyakazi anayeweza kuaminika kidogo. Nilimuona kijana mdogo hivi, apata umri wa miaka ishirini. Nilitoa noti ya shilingi mia na kumpa. Utafikiria kuwa huenda natumia pesa vibaya, lakini ukitaka cha uvunguni sharti uiname. Kijana kama huyo wakati wa mwambo kama huo ukimpa shilingi mia atakueleza hata yale aliyoyazungumza na mpenzi wake faraghani. Kijana huyo aligutuka sana hata akaniuliza, "He, unataka nini, pombe gani?".



"Hiyo fedha nimekupa, chukua ni yako. Sasa tafadhali naomba unielezee habari fulani fulani, Mbona chumba nambari hamsini hakina kitanda wala mtu?"



"Hicho chumba hakina mtu kwa sababu kinavuja kwa juu siku za mvua. Na siku hizi kuna manyunyu mengi".



"Kimeanza lini kuvuja?"



"Leo kiasi cha saa nne hivi kama unakumbuka kulikuwa na manyunyu,"



"Nambari hamsini na moja kulikuwa na mtu?"



"Ndiyo, mtu mmoja toka Uganda aitwae Fred, ndiye alikuwa amepanga humo kuanzia saa moja asubuhi."



"Kuna mtu yeyote aliyewahi kuingia chumba nambari hamsini kutoka nje wakati wa mchana?".



"Ndiyo, mtu mmoja aitwae Benny, alikuja na watu wengine watatu hivi. Waliingia kukitazama kama wanaweza kukiziba, lakini baada ya kukikagua sana walisema hawawezi, wakaenda zao. Sifahamu wanakaa wapi", alimaliza.



"Basi usimwambie mtu yeyote nilivyokuuliza."





Nilipotazama saa yangu, ilikuwa saa tisa na nusu. Nilitoka hapo baa na kukodisha gari hadi Starlight. Niliwakuta Robin na Sammy wakitungojea.



Robin hakuonekana mwenye furaha. Nadhani Sammy alikuwa amemweleza mambo yalivyokuwa. Halafu niliamua kupiga simu polisi ili waweze kushughulika na hizi maiti.



"Hapo ni Polisi?".



"Ndiyo Bwana, unataka nini?".



"Naweza kuzungumza na Polisi Inspekta Tsumah?. Tafadhali".



"Ngoja kidogo" alijibu.



"Hallo, huyu ni Polisi Inspekta Tsumah. Nani mwenzangu, na nikusaidie nini?"



"Mimi ni rafiki yako, ambaye ninazo habari za kukugutusha kidogo. Ni kwamba ziko maiti tatu katika Princess Hoteli chumba nambari 51. Nenda ukajionee mwenyewe. Miye sina uhusiano nazo. Kwa heri." nilikata simu kabla hajaweza kusema neno lolote.



Nilipiga simu kwa Chifu saa hiyo hiyo, nikimweleza kuwa awashauri maafisa wa polisi wasishugulike sana na mauaji yoyote yatakayotokea hapa Nairobi mpaka tutakapokuwa tumemaliza kazi yetu. Pia nilimweleza kuuawa kwa John.



Robini alitoa taarifa aliyokuwa amepewa na vijana wake juu ya Lulu. Alisema, "Baada ya wewe kutoka, Lulu naye alitoka. Mmoja wa vijana wangu alimfuata, na ilionekana Lulu alikwenda moja kwa moja hadi International Cassino. Alivyofika huko alisimama nje kwanza. Kisha alitoka kijana mmoja katika International Cassino na kuja kuonana naye. Alinyamaza alipokuwa akimeza mate.



"Walikaa hapo nje kwa muda. Kisha huyo kijana alimpa busu Lulu. Ilionekana kuwa Lulu alikuwa akimtegemea huyo kijana huko Starlight, lakini kijana huyo hakuonekana. Ilionyesha kuwa Lulu alijua kwamba huyo kijana mara nyingi alikuwa akienda Cassino. Alipofika hapo nje kumbe huyo kijana naye alikuwa akitoka. Kijana wangu alifikilia kuwa lazima wawe marafiki. Kijana huyo alionekana nadhifu sana, lakini macho yake yalionyesha uovu mwingi. Kijana wangu hakuweza kusikia waliyokuwa wakisema, ila alibuni kuwa walikuwa wakizungumzia juu ya kitu fulani kuhusiana na Starlight Klabu.



"Kijana wangu alingoja hapo mpaka walipokuwa wakiondoka. Walipoondoka, Kama alivyoripoti kijana wangu, waliingia katika gari moja Zephyr 6 nambari KKK 117. Walivyoanza safari ya kurudi mjini na Uhuru High Way naye aliwafuata. Walienda na kusimama nje ya Hoteli Intercontinental. Na Lulu alitoka nje. Alipokuwa akiingia hotelini, kijana wangu alimsikia Lulu akimuaga huyo kijana kwa sauti, "Kwa heri Benny."



Kusikia jina la Benny, nywele zangu zilisimama kidogo, kwani yule kijana wa Princess alikuwa pia ameniambia kama unakumbuka. Benny alikuwa amekuja kuchunguza kile chumba nambari 50. Katikati yangu na wewe nadhani Benny ana jambo hapo.



Nami nilimweleza mambo ambayo niliyapata kutoka kwa yule kijana wa hotelini. Nao walianza kumshuku Benny na Lulu pia. Maana kama nilivyosema awali. Kwamba wasichana waliovipande wote ni sumu mbaya sana.



Wote tulifikiria kwa tulikuwa tukianza kuona mwanga kidogo. Lakini hee, makubwa yalikuwa bado yanakuja. kwani kama huyo Benny na Lulu ndiyo wanacheza haya mambo lazima kuna kitu!

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Tuliondoka hapo nje ya Klabu na kila mtu akakodisha gari kwenda kulala. Tulikuwa tumepanga, kupigiana simu kesho yake asubuhi mnamo saa mbili. Robin alikuwa akilala New Avanue Hoteli.



Gari niliyokodisha ilinipeleka hadi hoteli Fransae. Kisha niliingia vichocholoni mpaka Embassy Hoteli. Kama mtu alikuwa akinifuata, angeweza kufikili kwamba nilikuwa nikilala hoteli Fransae. Niliingia chumbani kwangu ili nilale. Mawazo yangu yote yalikuwa juu ya mauaji ya John. Niliwaza kumuua huyo aliyemuua John iwapo muuaji huyo hatatangulia kiniua. Kitandani hapo chumbani, niliweka bastola yangu chini ya mto, kwani sikuweza kujua lini watu hao wangenifuata, maana wanaonekana kuwa wajuvi sana.



Asubuhi niliamshwa na mfagiaji, ambaye alikuwa anafagia nje ya mlango wangu. Kwa bahati mbaya akagonga mlango huo. Nilipotazama saa ilionyesha kuwa ilikuwa yapata saa mbili kasorobo. Nilikwenda kuoga, na kujiweka tayari kwa kazi ya mchana huo. Saa mbili kamili nilikuwa nimekwisha piga simu kwa Sammy na Robin.



Kabla sijapiga simu, Sammy alianza yeye kunipigia akisema, "hallo Willy, vipi? Umelala salama leo? Miye mwenzio nilikuwa na ndoto za ajabu na za kutisha. Nadhani kifo cha John bado kinanitisha. Sasa unasemaje, tuanzeje?"



"Sammy, nadhani haya tusiyazungumze kwenye simu, ila mpigie Robin simu umweleze mje hapa hoteli kwangu. Umeshapata kifungua kinywa ama vipi?"



"Bado sijapata, ila nategemea kupata sasa hivi."



"Vema, tutaonana saa tatu."



"Nililetewa kahawa na kuanza kunywa. Baridi ilikuwa kali sana... Ukungu ulikuwa umejaa kote. Siku ilianza kunitisha sana, hata kabla sijaanza kufanya lolote. Nilionekana mtu mwenye wasiwasi mwingi sana. Ungaliniangalia asubuhi hiyo hata wewe ungalinihurumia, ingawaje mimi si mtu wa kuhurumiwa. Ilipofika saa tatu. Sammy na Robin walifika. Mimi naona twende 'City Hall' maana maonyesho yanaanza leo saa tano. Na kama hamjui, leo ni sikukuu ya kufungua maonyesho. Kwa hiyo watu kote nchini wanapumzika hawaendi kazini. Na kwa sababu Lulu anasema ni mwonyeshaji mavazi, basi lazima atakuwepo. Na kama kweli Benny ni rafiki yake, hata yeye atakuwepo hapo 'City Hall' na kutokana na msongamano huenda tukafahamu lolote," alisema Robin.



'Gazeti la Daily National' lilikuja, na baada ya kuliangalia ilionekana mengi hayakuandikwa juu ya hivyo vifo. Maana waliandika tu ya kuwa "Watu watatu walikutwa wamekufa katika chumba kimoja Princess Hoteli. Polisi bado wanafanya uchunguzi," basi. Tulifikiria mkurugenzi wa usalama Kenya alifanya kama tulivyokuwa tumeomba.



Saa nne na nusu tuliondoka kuelekea City Hall. Sammy alibeba kamera na kuonekana kuwa mpiga picha hasa. Miye nilionekana kama mwandishi wa habari. Tulikuwa tumechukua vitambulisho vyetu. Tulipofika City Hall, baada ya kuonyesha vitambulisho vyetu, tulikuta siye tumepewa viti huko mbele karibu na jukwaa kusudi tuweze kuangalia na kuchukua picha vizuri. Mimi na Sammy tulikaa karibu karibu na Robin alikaa mbali kidogo nasi.



Robin alikuwa ameishafanya mpango na vijana wake kuwa karibu karibu katika huo ukumbi, kusudi ikiwa wataweza kuona lolote waweze kusaidia.



Kitu kilichokuwa kinaniuma ni kutaka kujua zilipokuwa hizo karatasi za siri. Pia wakati gani wamepanga kuzibadilisha. Na tatu wapi ambako haya mabadilishano yangefanyika. Mpaka hapo tulikuwa tumekwisha hakikisha kuwa Chifu alivyobuni itakuwa sawa. Maana mpaka hapo ilionekana ni watu wa Afrika Mashariki waliotuandama. Kule kujua kwao kwamba siye tumefika Nairobi na kuanza kuwasaka, kungefanya waharakishe kuzibadilisha hizo karatasi, kitu ambacho hatutaki kitokee. unaweza kuona mwenyewe jinsi muda ulivyokuwa mbaya. Akili zetu zilivurugika kama nini sijui.



"Hujambo mwananchi?" Nilisikia sauti kwa nyuma yangu ilinishtua sana kwa maana nilikuwa katika mawazo mengi. Nilipogeuka nikakuta ni mtu ninayemfahamu ambaye alikuwa muda mrefu sana Dar es Salaam. Huyu alikuwa Peter ambaye naye alikuwa mpigania uhuru na sasa akiwa ameletwa Nairobi kufanya kazi.



"Hallo Peter,habari? Mimi ni Joe Masanja nimekuja hapa kama mwandishi wa habari juu ya maonyesho ya mavazi. Na huyu ni Athumani Hassan, Mpiga picha".



Peter alijua nilikuwa na maana gani sababu ananijua, na anajua kazi yangu ni nini.



"Mmefika lini hapa. Lazima liwepo jambo alininong'oneza.



Kisha aliandika habari kwenye karatasi na kunipa. Humo aliandika maneno haya," Jee mmekuja kuchunguza kuhusu tukio la jana? Nimeambiwa na ofisi ya Dar es Salaam nisaidie. Kama ndivyo niko tayari kuwasaidia."



"Tulifika jana. Na hasa," nilijibu.



Peter alielewa, kisha alihama akaja kukaa na sisi. Alikaa upande wangu wa kulia na Sammy upande wa kushoto.



Baadaye nilimuona Lulu anaingia akiwa na Benny. Nilimuuliza Peter, "ati unawajua hawa?"



"Siwajui, ila tu nimewahi kumuona yule Benny katika mabaa fulani fulani tangu nifike hapa Nairobi. Kama ukipenda kujua jambo lolote juu yake hiyo ni kazi rahisi. Ninaweza kukupatia habari kabla ya usiku wa manane leo."



"Nitafurahi sana ukifanya hivyo na watu wako."



Peter alioneka mwenye kuhudhunishwa sana na jambo hili akiwa kama mpigania uhuru. Baadaye Lina naye aliingia. Alikuwa peke yake kama kawaida. "Ulitaka kumuona yule? Nilimuuliza Peter.



Ndiyo. Yeye ni Lina Samson."

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Lina alikuwa msichana tofauti sana na wasichana wengine. Sura yake ilikuwa ya kupendeza vya kutosha, kama nilivyosema awali. Lakini licha ya Lina kuwa mzuri wa sifa hivyo, hakufua dafu kwa Lulu, kwani Lulu alikuwa 'Lulu' kweli. Pia Peter alisema utamkuta Lina siku zote peke yake mwenye mabaa akinywa soda akichanganya na 'Babycham'. Hivi ndivyo hata mimi nilimkuta usiku uliopita. Lina alituona akaja moja kwa moja kutusalimia. Kisha akanipigia kope akaenda kukaa mbali nasi kidogo.



Wakati Benny alipoingia na Lulu kila mtu aligeuka kuwaangalia. Lulu alitembea kwa maringo sana na Benny alionekana akifurahia kuona kila mtu akimwangalia wakati wakifuatana na mrembo huyo wa kushtua. Hata mimi nilimuonea wivu. Maana nilitamani niwe mimi badala yake nitembee na mrembo huyo. Lina alimwangalia sana Lulu. Nikaona huenda alikuwa pia akimuonea haya Lulu.



Nilitambua kuwa Lina anamfahamu Benny, kwani Benny alipokuwa anapita na Lulu, alipomuona Lina amekaa karibu na mahali walipokuwa wakipita, alitazama chini. Kwa hiyo niliona itakuwa vizuri kama nitafanya urafiki na Lina maana naweza kupata msingi mdogo wa kutusaidia. Pia niliona Lina angeweza kusikilizana na mimi, kwani kama nilivyosema alinipigia kope kuonyesha dalili ya urafiki.



Maonyesho yalipoanza wanawake walianza kutoka mmoja mmoja wakionyesha mitindo ya kila aina. Kulikuwa na wanawake kutoka karibu kote Ulimwenguni wakitoa mitindo mbali mbali. Niliandika kikaratasi na kumpa Sammy akiangushe katika mapaja ya Lina, wakati akijifanya kama kwamba anatafuta mahali pazuri kwa kupiga picha. Niliandika, "Tafadhali tuonane nje, kwenye mlango mkubwa, kama dakika kumi kabla ya watu wote kutoka. angalia watu wasifahamu unaningoja mimi************".



Sammy alikiangusha kama nilivyomueleza. Baada ya kusoma bila mtu kujua aliniangalia na kutikisa kichwa, akionyesha kuwa amekubali. naye alianza kuandika kwenye hicho kikaratasi. Akakitupa mbele ya Sammy. Alipokuwa anarudi. Sammy alijifanya ameangusha kasha la 'Film', akainama na kukiokota hicho kikaratasi pamoja na kasha la 'film' yake. Niliposoma nikakuta maneno haya. *************"Ndani ya gari langu jeusi namba No. KKT 581 - Mazda Delux - kulia mwa mlango mkubwa," basi niliona mambo yote yamekuwa kama nilivyopanga. Lakini ukavu wa macho ya Lina ulinitisha kiasi cha kwamba woga uliniingia kidogo. Lakini kwa sababu sikuwa mwoga kama wewe, sikujali lolote litalotokea baadae.



Lulu alijitokeza. Alipotokea kwenye jukwaa kila mtu alipiga kelele, kwa vifijo na ushangiliaji wa ajabu. Lulu aling'aa kama nyota. Alionyesha mtindo wake unaoitwa 'Popcom'. Wachukuaji wa picha walichua picha kwa fujo sana.



Alipokuwa anarudi kwenye chumba wanachotokea. Robin alipita karibu yangu na kudondosha kikarasi. Nikakisoma kilikuwa kimeandikwa "Mjiangalie sana, maana yametokea mauaji mawili tayari humu ndani", wakati Lulu alipotoka na watu walipokuwa wakipiga kelele na kushangilia vibaya sana, vijana wetu tuliokuwa tumewaweka kuviziavizia, wawili wao wameuawa. Inaonekana waliona jambo fulani ambalo limewaponza. Mueleze na Athumani, laa zivyo na siye tutakufa".



Lo wasiwasi ulinizidi sana. Sammy alipokuja karibu yangu nilimueleza mambo yalivyokuwa. Zilikuwa zimebaki kama dakika kumi na tano hivi maonyesho ya asubuhi yaishe. Hivyo tukafungashafungasha vijitabu vyetu tuondoke. Tulimuaga Peter baada ya kumweleza ninapokaa. Tulitazama huku na huku kwa mashaka makubwa sana. Nadhani hata wewe unaweza kufikiria mawazo tuliyokuwa nayo.



Tulipofika mlangoni, nilibahatisha kumuona Benny amesimama na kijana fulani akimueleza mambo fulani fulani na huku akitutizama kwa usiri mno. Nilijua alikuwa akimuambia huyo kijana atufuate. Hivyo nilimueleza Sammy abaki nyuma kidogo ili niweze kuwapoteza wasije wakajua ninaondoka na Lina.



Peter alikuwa kwenye dirisha moja la 'Hall" na akaniona nilipokuwa nikiingia katika gari la Lina. Akanipungia mkono. Nadhani aliweza kupata nafasi ya kukisoma kikaratasi cha Lina. Sikujali Peter kufahamu hayo, kwani na yeye ni mtu wetu.



"Mtu yoyote amekuona?"



"Hapana, uenda wamekuona wewe" alijibu.



"Sidhani kama wameniona"



Lina alitia moto tukaondoka. "Tupitie njia ipi?" aliuliza.



"Twende moja kwa moja, mpaka Embassy Hoteli."



Lina alivuta gari mpaka tukaingia Kenyatta Avenue. Nilipotazama nyuma, niliona gari moja kama kwamba linatufuata. Kutaka kuhakikisha nilimueleza Lina badala ya kuingia Koinange akate kona na kuingia uhuru High Way. Halafu aingie Haile Selassie Road. Gavament Road ndipo turudi Kenyatta Avenue. Kisha tuendelee na safari yetu. Kusema hili gari lilikuwa linatufuata maana kuzunguka kote huku nalo lilikuwa bado linazunguka kutufuata tu. Tulipofika kwenye kona ya Kenyatta Avenue nilimwambia Lina asimame, aliposimama hilo gari nalo likasimama karibu sana nasi. Nilitoka nje nikamfuata dereva wa gari hilo.

"Sikiliza bwana mdogo, Miye sitaki kufuatwafuatwa. Sikuzoea mambo hayo. Na kama hutaki meno yako zidi kunifuata. Kamwambie huyo mume wako aliyekutuma kuwa kama anataka kunitafuta aje yeye mwenyewe ajionee. Kama unataka usalama tia gari lako moto uende zako."

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Kijana huyo hakuwa na la kufanya ila kufanya kama nilivyomwambia. akaenda zake. Nilirudi katika gari la Lina akaendesha mpaka Embassy Hoteli.



"Sikiliza Lina, nenda ukasimamishe gari hili mbali na Embassy Hoteli kusudi hawa wahaini wasijue tuko hapa wakatufuata"



Baada ya kuweka gari Lina alikuja tukapanda mpaka kwenye chumba changu. "Sijui kwa nini naonekana kukupenda, maana tangu jana mle Princess Hoteli, baada ya kutoka na kukuacha humo, usiku mzima sikulala ila kukufikiria wewe tu." Alisema Lina hali akijilaza.



"Oh Joe, mpenzi nakupenda sana ingawaje unaweza kuniona kuwa miye malaya kwa kukufuata baada ya kuonana siku moja tu. Lakini lazima ujue kuwa mtu unaweza kuwa hujapenda, lakini akaja mtu mgeni ukampenda kufa. Hapa Nairobi nimeishawahi kufanya mapenzi na mtu mmoja tu, ambaye anaitwa Benny Makunda. Lakini hata siku moja sikuweza kukosa usingizi juu yake, kama nilivyokosa juu yako jana. Ningejua unakaa hapa basi tu ningekufuata."



"Waaa, unasema kweli ama tu kunidhihaki? Hata mimi nimekupenda Lina. Tangu jana tabia yako ya utulivu na kiburiburi niliipenda sana. Maana mimi napenda watu kama hao hasa wakiwa wasichana"



Loo! Hapa niliona mambo yanakorogana sana Benny aliwahi kuwa mpenzi wa Lina. Na Benny ndiye tuliyekuwa tunamashaka naye. Huyu kijana anaonekana ni 'Champion' kwa wanawake, kwani sasa anatembea na Lulu. "Huyu msichana Lina ananitania ama vipi." ndiyo sasa yalikuwa mawazo yangu. "Lakini yote hayo nitafahamu muda si mrefu kwani naweza kumusoma msichana kama Lina Vizuri sana."



"Kumbe unamfahamu Benny, hata amewahi kuwa mpenzi wako?" Nilimuuliza.



"Ndiyo," alijibu.



"Mmeachana tangu lini?"



"Kuna huyu msichana wanayemwita Lulu. Msichana huyu anatoka Uganda na huwa yuko huku mara nyingi sana. Sura yake kama ulivyomuona inavutia wavulana wengi sana. Alipokuja huku mwezi wa jana Benny alimuona, na wakaanza mapenzi. Mwishowe Benny hakunijali tena. Nami kwa tabia yangu nikaona siwezi kupenda mtu ambaye hapendeki.



"Kwanza nilimuonya Benny asitembee na Lulu kwani Lulu ingawaje ni mzuri kiasi cha kutisha namna ile, lakini ni hatari sana kwa mambo ya ukahaba. Lakini baada ya muda mfupi Lulu alirejea Uganda. Benny akarudi sasa. Lakini miye sikumtaka tena.



"Benny ana fedha na ana fedha nyingi. anazitoa wapi sijui, lakini ana fedha. Kazi yake ni dereva wa taksi tu. Anaendesha taksi yake moja 'Mercedes Benz'. Nilipokataa Benny alinibembeleza sana lakini nikakataa tu bado. Aliniahidi kuwa angelininunulia gari moja aina ya 'Citron' mwezi huu, maana atakuwa 'Giriki' mwezi huu. Miye nilizidi kukataa tu. Na nilikuwa nimeapa hata siku moja sitafanya mapenzi na mvulana tena. Nilikuwa nafikiria kwenda kuwa mtawa. Bahati nzuri au mbaya ndipo akaja huyu kijana ambaye amenifanya hata sikuweza kulala. Oh, kweli mama aliniambia usimpende mgeni, lakini mimi hata, nitakupenda tu."alimalizia Lina.



Bado mimi sikumwamini hata punje.



"Benny alikwambia hiyo pesa angetoa wapi?" Nilimuuliza.



Alisema ati ana rafiki zake huko ng'ambo ambao wangemletea fedha hiyo. Benny anafahamiana na wazungu wengi sana," alisema kwa mashaka kidogo.



Ubaya wa huyu msichana ni kuwa huwezi kumwelewa hata kidogo kwani anaposema, husema kwa utulivu mno hivyo kwamba huwezi kumtambua yupo upande upi.



"Unaweza kuwatambua wazungu hawa ukiwaona?"



"La, wengi wao wamerudi kwao. Ndiyo sababu nakueleza kuwa, watamtumia pesa kutoka ng'ambo waliko," alijibu.



"Unafikiria ni Wazungu kutoka upande gani?"



"Sijui maana mimi nilikuwa sihusiani nao sana."



"Ni wanaume au wanawake?" Nilimwuliza huku nikijifanya siyajali sana mazungumzo yake haya.



"Lo, Joe, mimi sikuja hapa kujibu maswali juu ya Benny. Mimi nimekuja kwa sababu napenda kuzungumza juu ya maisha yangu na wewe na kufanya mapenzi. Kama unatafuta wanawake wa Kizungu, ambao Benny hutembea nao, ni rahisi sana kuwapata hapa Nairobi. Na kwa vile wengi wamekuja kwenye maonyesho, nenda tu ujipige utapata," alijibu kwa uchungu sana na hasira.



"Si hivyo Lina. Sina haja na wanawake wa kizungu, ila tu nilitaka kufahamu mengi juu ya Benny, kwani anaonekana anawakosha sana wasichana. Mtu wa kuweza kumuacha msichana wa haiba kama wewe, lazima awe mwamba hasa."



"Lakini unanipenda kweli Joe?" Alisema huku machozi yakimtoka.



"Ninakupenda sana Lina. Na sasa ninaanza kukuelewa na kukupenda zaidi. Je. Benny anakaa wapi?"



"Benny anakaa huko Westlands, karibu na maduka ya Westlands. Nyumba "plot No. 3" pembeni mwa Nakuru Road, baada ya kuvuka Motel Agip. Au kwa urahisi karibu na Sclaters Hostel."

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Mpenzi Lina, nataka kukuambia ukweli sasa. Mimi si Joe Masanja, mimi ni Willy, Willy Gamba." Lina alikuwa amelala kwenye kitanda lakini nilipotaja hilo jina, aliruka na kusimama mbele yangu huku anaonyesha hali ya kushangaa sana.



"Mimi ni mpelelezi wa Idara ya Uchunguzi ya Tanzania." Nilitoa kitambulisho changu cha upelelezi. "Usishtuke Lina, Kaa chini na huenda toka sasa tutaelewana vizuri zaidi. Na huenda toka sasa ukanisaidia." Nilienda kukaa karibu naye hapo kitandani.



Alinivuta akaanza kufungua tai yangu, kisha shati langu, halafu suruali yangu... tukajilaza.



ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog