Search This Blog

Saturday 5 November 2022

MAUAJI YALIYOJAA UTATA - 5

 





    Simulizi : Mauaji Yaliyojaa Utata

    Sehemu Ya Tano (5)





    Kulikuwa na watu wawili tu waliokuwa wakikizuzua kichwa cha Bwana Seppy kila siku, mtu wa kwanza kabisa alikuwa Benjamin na wa pili alikuwa msichana Stacie ambaye kwa kipindi kifupi tu aliuteka moyo wake na kuuendesha alivyotaka.

    Hakutulia, kila wakati alionekana kuwa mtu mwenye mawazo mengi, alichanganyikiwa na wakati mwingine alihisi kama angeweza kupoteza maisha kutokana na jinsi alivyokuwa na mawazo lukuki kichwani mwake.

    Kwa wakati huo alikuwa akisubiri habari njema kutoka kwa vijana wake aliowatuma kumteka Benjamin na kuja kumuua kwa mkono wake. Tangu vijana hao walipoondoka mpaka muda huo, hakuwa amepata taarifa yoyote ile kitu kilichomshangaza sana.

    Dracula, mmoja wa vijana wake alikuwa mtu makini sana, kila alipomtuma, alikuwa mleta taarifa mzuri sana, hata kabla hajauliza kilichokuwa kimeendelea, tayari alimpa taarifa lakini siku hiyo, hali ilionekana kuwa tofauti kabisa, kila alipompigia simu Dracula, ilipatikana, ila haikupokelewa kitu kilichomtia wasiwasi mkubwa.

    “Kuna nini? Mbona hapokei simu?” alijiuliza huku akikosa jibu kabisa.

    Aliendelea kusubiri zaidi kwani kila alipopiga simu majibu yalikuwa yaleyale kwamba simu haikupokelewa.

    Baada ya saa moja ndipo akaona kulikuwa na simu iliyoingia katika simu yake, moja kwa moja akayapeleka macho yake katika simu ile, namba aliyokutana nayo ilikuwa ni ya Dracula, harakaharaka akaipokea.

    “Mmefikia wapi?” lilikuwa Swali lake la kwanza kabisa hata kabla ya salamu.”Ametukimbia...”

    “Amewakimbia, yaani kirahisi tu?”

    “Hapana mkuu! Tulikutana na tatizo, kulikuwa na maofisa wa FBI nao walikuja kumchukua, tukawa tunarushiana risasi, tumepoteza mwenzetu mmoja ila FBI wote wapo chini,” alisema Dracula.

    “Kwa hiyo Benjamin mmemkosa?”

    “Tulimpata, tulikuwa naye ila mapigano yalivyoanza, akapata nafasi ya kukimbia, ila tunaye mpenzi wake hapa,” alisema Benjamin.

    “Nani? Vivian?”

    “Ndiyo!”

    “Mleteni huyohuyo.”

    Hakutaka kusikiliza mazungumzo zaidi, alichokifanya ni kukata simu huku akiwa kwenye hasira kali, moyo wake ulikasirika, kitendo cha vijana wake kumpata Benjamin na kisha kuwatoroka kwake kilionekana kuwa kama uzembe mkubwa hata kama walikuwa wamezungukwa na maadui.

    Kwa sababu Vivian alipatikana, kwake hakukuwa na tatizo, msichana huyo alikuwa muhimu kwani aliamini kama angekuwa naye basi ilikuwa ni lazima Benjamin ajipeleke kwani bila kufanya hivyo aliahidi kumuua Vivia ili kumtia hofu kijana huyo.

    Wala haukupita muda mrefu, Vivian alikuwa mbele ya Bwana Seppy, kwanza akamwangalia msichana huyo, hakumpenda kwa sababu mpenzi wake alimsumbua sana. Akamwamuru Dracula amuweke kwenye kochi na yeye kuanza kuzungumza naye.

    “Ben yupo wapi?” aliuliza mzee huyo.

    “Sijui chochote kile,” alijibu Vivian huku akionekana kuwa na kiburi fulani.

    “Unanificha?”

    “Hapana! Waulize vijana wako, mimi sijui chochote kile,” alisema Vivian kwa ujasiri mkubwa.

    Bwana Seppy hakutaka kuuliza swali jingine, alichokifanya ni kuamuru msichana huyo achukuliwe na kupelekwa katika chumba kimoja kilichokuwa ndani ya nyumba hiyo, chumba hicho kilikuwa na giza kubwa huku kukiwa na buibui wengi.

    Kilikuwa chumba chenye mateso makali, watu wengi waliojifanya jeuri, walichukuliwa na kuingizwa ndani ya chumba hicho na kuachwa kwa siku kadhaa.

    “Nisikilize Dracula,” alisema Bwana Seppy.

    “Ndiyo mkuu!”

    “Unamfahamu Stacie?”

    “Huyu mrembo wa dunia tuliyekwenda kumuona siku ile?”

    “Ndiyo!”

    “Amefanyaje?”

    “Ninaitaka roho yake!”

    “Kwa nini?”

    “Dracula! Tangu lini umeniuliza sababu? Nimekwambia ninaitaka roho yake, unaniuliza kwa nini! Unataka nikujibu nini?” aliuliza Bwana Seppy huku akionekana kuwa na hasira kubwa.

    “Samahani mkuu! Tumuue kama kawaida au kivingine?”

    “Kama kawaida!”

    “Sawa.”

    Huo ndiyo ulikuwa uamuzi aliokuwa ameufikia, hakutaka tena kuwa na huruma, alimpenda msichana Stacie, alimwambia lakini mwisho wa siku msichana huyo akamletea mapozi na kumkataa.

    Hilo lilimkasirisha na ndiyo ilikuwa sababu ya kupanga mauaji, hakutaka kuumizwa moyoni mwake, kitendo cha kukataliwa kilimfanya kuwa na chuki kali dhidi ya Stacie, alijijua kwamba alikuwa na fedha nyingi hivyo kuwa na uhuru wa kuwa na msichana yeyote yule, sasa kwa nini msichana huyo amkatae?

    Vijana wake wakaondoka mahali hapo, ilikuwa ni lazima kummaliza msichana Stacie kama walivyowamaliza watu wengine ambao walimkwaza Bwana Seppy ambaye alikuwa na utajiri mkubwa mno kipindi hicho.

    Kabla ya yote, kitu cha kwanza kabisa ni kuanza kutafuta msichana huyo alikuwa sehemu gani.







    Maisha yalibadilika kabisa, kilichokuwa mbele ya Stacie kilikuwa ni kutengeneza pesa tu. Mikataba iliendelea kumiminika, aliisaini tena kwa kiasi kikubwa cha fedha. Alijiona kuwa tajiri mkubwa hapo baadaye, watu walizidi kumpapatikia kwa sababu alikuwa msichana mrembo, mwenye mvuto wa ajabu ambapo kila mwanaume alitamani sana kuwa naye.

    Hakuwa mwepesi, alitaka kutengeneza pesa kwanza kabla ya kuamua kuwa na mwanaume fulani. Mtu ambaye alikuwa akimfikiria kipindi hicho alikuwa mwanaume mmoja tu, huyu aliitwa Alan, mwanaume aliyewahi kuwa naye utotoni.

    Siku zikaendelea kukatika, akasahau kama alitakiwa kurudi nchini Australia, kama walivyokuwa mastaa wengine, naye akatokomea nchini Marekani kwani ndipo kulipokuwa na ishu nyingi za pesa, kurudi nchini kwake isingewezekana tena.

    Baada ya miezi kadhaa, akaitwa kwa ajili ya kuwa balozi wa watoto katika shirika la Umoja wa Mataifa kupitia UNICEF. Kazi kubwa ilikuwa ni kuzunguka duniani kote, kukutana na wanawake na watoto waliokuwa na matatizo kiafya na kuzungumza nao huku kiasi kikubwa cha dawa kikiwa kimeandaliwa.

    Kichwa chake hakikumfikiria Bwana Seppy, hakujua ni maumivu makali kiasi gani aliyomuachia mzee huyo, aliendelea na maisha yake kama kawaida huku kila alipokwenda, watu walimheshimu mno.

    “Kuna simu nilipigiwa,” alisema meneja wake, Robert.

    “Na nani?”

    “Mkurugenzi wa Google.”

    “Amesemaje?”

    “Anataka kuingia mkataba na wewe kwa ajili ya kufanya matangazo zaidi juu ya programu mpya wanayotarajia kuiweka katika simu zote zinazotumia android,” alijibu.

    “Mmh! Wamesema wanaweza kutoa kama kiasi gani?”

    “Sijajua ila si chini ya dola milioni hamsini,” alijibu meneja huyo, kiasi hicho kilikuwa ni zaidi ya shilingi bilioni mia moja.

    “Sawa! Tukitoka huku, tutaonana nao tuwasikie, ila nina furaha sana,” alisema Stacie huku akiachia tabasamu pana.

    Wakati huo walikuwa safarini kuelekea nchini Japan, alikuwa ameingia mkataba na kampuni ya kutengeneza matairi ya Yokohama, alitakiwa kwenda huko haraka iwezekanavyo, hakutaka kuchelewa kwani kiasi alichowekewa kilikuwa kikubwa mno, hivyo akafanya hivyo.

    Ndani ya ndege, muda wote alikuwa mtu mwenye mawazo tele, hakuamini kama kile kilichokuwa kikiendelea kiliendelea katika maisha yake. Hawakuchukua muda mrefu ndege ikaanza kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Tokyo.

    Hapo, kulikuwa na maofisa wa Yokohama ambao walitumwa kumpokea msichana huyo mrembo. Walipotoka tu nje ya uwanja huo, kundi kubwa la waandishi wa habari wakaanza kuwasogelea na kuwapiga picha.

    Walifanya kile walichokuwa wameitiwa na baada ya siku mbili, safari ya kurudi nchini Marekani ikaanza. Kichwani mwake alikuwa akifikiria mkataba aliotaka kuingia nao na Kampuni ya Google. Wakati mwingine aliiona ndege hiyo ikichelewa kutua, alitamani kufika nchini Marekani na hatimaye asaini mkataba uliokuwa mbele yake.

    Walichukua saa kumi na sita mpaka kufika nchini Marekani ambapo ndege ikatua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa JFK uliokuwa jijini New York.

    “Wamesema wapo jijini Las Vegas,” alisema Robert.

    “Las Vegas?”

    “Ndiyo!”

    “Tunatakiwa kupumzika. Mpigie simu Alejandro na umwambie ajiandae, kesho tunakwenda huko,” alisema Stacie na Robert kufanya hivyo.

    Usiku wa siku hiyo hakulala vizuri, kila alipogeuka, alizifikiria fedha ambazo aliahidiwa kupewa kama tu angesaini mkataba wa kuitangaza kampuni hiyo.

    Asubuhi ilipofika, akaamka, tayari tiketi zilishakatwa na hivyo kuonana na Alejandro kisha kuanza safari ya kuelekea huko Nevada katika Jiji la Las Vegas.

    Baada ya saa mbili, ndege ikaanza kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa McCarran. Kitendo cha kufika katika jiji hilo tu kikampa uhakika wa kuondoka na mamilioni ya dola.

    Walipofika nje, wakapanda ndani ya gari maalumu waliloandaliwa na kisha kuelekea katika Hoteli ya Vikings Hill. Wakapelekwa katika vyumba walivyotakiwa kulala. Siku hiyo akalala hotelini pasipo kujua kama kulikuwa na watu walitumwa kwa ajili ya kuichukua roho yake tu.

    ****

    Kujua Stacie alikuwa wapi kipindi hicho halikuwa jambo kubwa, wakapata taarifa kwamba msichana huyo alikuwa safarini akielekea nchini Japan kwa ajili ya kufanya matangazo ya biashara na kuwekeana mkataba na Kampuni ya Yokohama iliyokuwa ikitengeneza matairi ya magari na ndege.

    Hawakutaka kuelekea nchini humo kufanya mauaji, kwa kuwa kipindi hicho ilikuwa ni lazima afike nchini Marekani kwa ajili ya shughuli zake, walihakikisha wanamsubiri ili siku akiingia, kama kawaida wafanye kile walichoambiwa.

    Walijiandaa kwa kila kilichokuwa kikiendelea, waliwaweka watu tayari kwa ajili ya kufuatilia ishu nzima ya Stacie na baada ya kuondoka nchini Japan siku mbili baadaye, walipewa taarifa nzima kwamba msichana huyo alitakiwa kwenda Las Vegas kwa kuwa Kampuni ya Google walitaka kufanya naye biashara kwa kusaini mkataba mnono ambao ungewatangaza.

    “Alisema atafikia kwenye hoteli gani?’ aliuliza Dracula.

    “Bado sijajua, ila nikijua tu, nitawapeni taarifa,” alisema mtoa taarifa.

    Huo haukuwa mwisho, waliendelea kuzipokea taarifa hiyo na taarifa ya mwisho kabisa kuwafikia ilisema kwamba msichana huyo angefikia katika Hoteli ya Vikings Hill.

    “Ni lazima twende huko kabla yake,” alisema Dracula.

    “Hakuna tatizo.”

    Baada ya saa mbili, Dracula na wenzake wawili walikuwa ndani ya ndege wakielekea jijini Las Vegas. Ilikuwa ni lazima kufanikisha kile walichoambiwa kwani bila kufanya hivyo, walijua kwamba kungekuwa na tatizo kubwa kwani Bwana Seppy hakutaka washindwe kwenye jambo lolote lile.

    Walipofika, wakateremka kwenye ndege na moja kwa moja kuelekea nje ambapo wakakodi taksi iliyowapeleka mpaka katika hoteli hiyo ya kifahari ambapo ndani yake kulikuwa na Cassino iliyokuwa na michezo mingi ya kamari.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hawakuacha kuwasiliana na kijana aliyekuwa akiwapa maelekezo, aliwaambia kwamba tayari msichana huyo aliingia jijini New York na hivyo kesho asubuhi angeanza safari ya kwenda Las Vegas ambapo tayari aliweka oda ya vyumba ndani ya hoteli hiyo.

    “Tutafanikiwa, nilihisi kwamba tungekuwa na ugumu, ila inaonekana kuwa kazi nyepesi sana,” alisema Dracula.

    “Kwa hiyo tumuue kama wale wengine?”

    “Ndiyo! Hayo ni maelekezo niliyopewa na mzee.”

    “Basi hakuna tatizo.

    Walichokifanya ni kwenda kutembea, walizunguka sehemu mbalimbali kwa ajili ya kula raha tu, walikuwa na fedha hivyo kila kitu walichokifanya kiligharimu fedha kitu ambacho wala hawakuwa na tatizo nacho kwani kama fedha, walikuwa nazo za kutosha tu.

    Muda mwingi walikuwa wakiifikiria kazi hiyo, walitakiwa kupanga mipango kabambe, walijua kwamba kulikuwa na kamera ndani ya hoteli hiyo ila walitakiwa kufanya kila linalowezekana kuhakikisha hawakamatwi na mtu yeyote yule.

    Walizunguka kwa zaidi ya saa moja na nusu ndipo wakarudi hotelini ambapo baada ya kula, wakalala huku wakiisubiri siku inayofuatia kwa hamu kubwa.

    Asubuhi ilipofika, wakaelekea katika mgahawa uliokuwa chini na kupata kifungua kinywa. Huko ndipo waliposikia taarifa za ujio wa msichana Stacie kwamba angefikia katika hoteli hiyo siku hiyo.

    Watu kutoka sehemu mbalimbali walianza kufika ndani ya hoteli hiyo, kila mmoja alitaka kumuona msichana huyo, wengi walimuona katika sehemu mbalimbali, hasa kwenye televisheni na majarida, siku hiyo walitaka kumuona ana kwa ana.

    “Kuna kitu jamani,” alisema kijana mmoja.

    “Kitu gani.”

    “Nina wazo. Nadhani tukitumia njia kama tuliyowaua watu huko nyuma tutashindwa kwani watu wanajua hivyo tunaweza kukamatwa,” alisema kijana huyo.

    “Wewe unataka tufanye nini?”

    “Ni lazima tumlevye huyu msichana.”

    “Kivipi?”

    “Kwa kutumia madawa ya usingizi. Tutumieni hata Phenometriphone, sumu yenye nguvu ambayo ikimpata mtu kwenye ngozi yake, ndani ya dakika arobaini, atalewa na kulala kwa usingizi mzito,” alisema kijana huyo.

    “Baada ya hapo?” aliuliza Dracula.

    “Ndipo tutamuua kwa kuingia chumbani kwake bila kipingamizi,” alisema kijana huyo.

    Wazo alilolitoa liliungwa mkono na kila mtu, hakukuwa na mtu aliyekataa, kumlevya msichana huyo kabla ya kumuua lilionekana kuwa jambo jema ambalo kama wangelifanya, lingewapa urahisi, na wasingeweza kugundulika kwa urahisi.

    Kitu walichokifanya ni kuanza kutafuta sumu hiyo. Waliuona ugumu uliokuwepo mbele yao, isingekuwa kazi nyepesi kuuziwa dawa hiyo pasipo kuwa na kibali kutoka kwa daktari ila kwa kuwa walikuwa na fedha, waliamini kwamba kila kitu kingekuwa chepesi.

    Wakaondoka na kwenda kwenye duka la dawa, Dracula ndiye aliyekuwa mteja wa kununua sumu hiyo, alipofika kwenye duka moja la dawa, muuzaji alikataa kumuuzia, alichokifanya ni kutoa noti za dola, akaweka mezani dola elfu moja, harakaharaka akapewa sumu aliyoitaka na glavu.

    “Ila usinichome,” alisema muuzaji huyo.

    “Usijali.”

    Dracula akaondoka na kurudi hotelini, huko akaonana na marafiki zake na kuwaambia kile kilichoendelea ambapo alikuwa na sumu hiyo iliyokuwa kwenye kikopo kidogo.

    Aliwaambia kwamba walitakiwa kuwa na gravu, alikuja nazo hivyo kujiandaa huku yeye ndiye aliyetakiwa kumpaka msichana Stacie sumu ile.

    “Tujadiliane, tutampaka vipi?” aliuliza Dracula.

    “Kazi nyepesi sana, niachie mimi. Kitu cha msingi, yule kijana anayepokea mabegi watu wanaokuja hotelini, ile nafasi tunatakiwa kuwa nayo sisi,” alisema kijana aliyetoa wazo, kijana mwenye akili nyingi, huyu aliitwa Stephen, ila alipendwa kuitwa Steph.

    Walichokifanya ni kusubiri, waliposikia kwamba msichana huyu alikuwa kwenye ndege, wakawasiliana na kijana aliyekuwa akihusika kupokea wageni na kumwambia kwamba walitaka kuzungumza naye, kijana yule pasipo kujua hatari iliyokuwepo, akawafuata chumbani, hukohuko wakamfunga kamba miguuni na mikononi huku wakimuwekea plasta kubwa mdomoni.

    Steph akachukua mavazi ya kijana yule na kuyavaa kisha kutoka ndani ya chumba hicho. Kwa kuwa hoteli ilikuwa kubwa, tena ikiwa na wafanyakazi wengi ilikuwa kazi ngumu sana kugundua kwamba kijana huyo hakuwa mmoja wa wafanyakazi.

    Tayari mkono wake wa kulia aliupaka sumu ile na aliyekuwa akimsubiri alikuwa Stacie tu. Baada ya dakika ishirini, kelele za watu zikaanza kusikika kuonyesha kwamba msichana huyo alikuwa akikaribia kuingia mahali hapo.

    Harakaharaka Steph akapiga hatua, gari liliposimama, akaufungua mlango, watu wakawa wanampiga picha Stacie, alipoteremka tu, akampa mkono, wakasalimia tena kwa kushika kiuhakika kana kwamba walikuwa wakifahamiana, baada ya hapo, akachukua mabegi yake huku tayari akiwa amekwishampaka sumu ile Stacie.

    “Tayari! Kwisha habari yake,” alisema Steph huku akiwa ameshika mabegi ya Stacie aliyekuwa akiwasalimiana na mashabiki zake, alipofika mapokezi, mizigo akaitelekeza, akapandisha juu mpaka katika chumba walichokuwepo wenzake na yeye kuingia.

    “Imekuwaje?” aliuliza Dracula.

    “Kila kitu tayari,” alijibu Steph huku akitoa tabasamu pana.







    Kwa kumwangalia, Stacie alionekana kuwa na furaha tele, hakuamini kama kulikuwa na watu waliokuwa wakimpenda kama ilivyokuwa, kila alipowaangalia, moyo wake ulikuwa na furaha tele.

    Ni kweli alipendwa lakini watu waliojitokeza hotelini siku hiyo walikuwa wengi, ilimshangaza, alichokifanya baada ya kusaini vitabu vya mashabiki hao ni kuondoka na kuelekea ndani ya hoteli hiyo ambapo tayari kilikwishaandaliwa.

    Alipokaa kitandani na kuanza kuvua nguo zake, akaanza kujisikia hali ya tofauti, mwili ulichoka na macho yake yakawa mazito, alishindwa kujua nini kiliendelea kwani dakika chache zilizopita wakati akiingia ndani ya hoteli hiyo, alijisikia vizuri kabisa, hakuwa na uchovu wowote ule.

    Akapuuzia, akaendelea kuvua nguo zake lakini ghafla akajikuta akilala kitandani, usingizi mzito ukampitia, hakujua ni kitu gani kiliendelea baada ya hapo.

    Dracula na vijana wake waliokuwa ndani ya kile chumba, harakaharaka wakatoka na kuelekea chumbani kule, walijua kwamba mpaka muda huo msichana Stacie alikuwa amelala kutokana na kuzidiwa sumu ile aliyopakwa.

    Mlango haukuwa umefungwa, ulikuwa wazi walichokifanya ni kuufungua na kuingia ndani. Walimuona msichana huyo akiwa kitandani, hakuwa akijitambua, alizidiwa na sumu aliyokuwa amewekewa, hawakutaka kuchelewa, walichokifanya ni kuanza kumnyonga hapohapo kitandani, tena kwa kumziba pua na mdomo.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wala hawakupata ushindani wowote ule, walifanikiwa kufanya walichotaka kukifanya kwa asilimia mia moja, baada ya kuhakikisha mapigo ya moyo yamesimama, wakachukua dawa za kulevya na bomba la sindano kisha kumchoma kwenye mkono wake na kuziweka alama za vidole vya Benjamin kwa kutumia plastini yenye unyevuunyevu kama kawaida, baada ya hapo wakaacha fedha walizotakiwa kuziacha na kisha kuondoka mahali hapo huku wakiwa wamefanikiwa.

    Taarifa zilisikika usiku uleule baada ya mhudumu kufika ndani ya chumba hicho kwa ajili ya kumhudumia msichana huyo. Alipofika, akaanza kuugonga mlango ili afunguliwe lakini hakukuwa na sauti yoyote iliyosikika kutoka ndani, ukimya mkubwa ulikuwa umetawala.

    Alichokifanya mhudumu huyo ni kwenda mapokezini ambapo huko akahitaji dada wa hapo apige simu katika chumba hicho ili azungumze na Stacie na kumwambia kwamba walitaka kumhudumia kwa kumpelekea chakula.

    Simu ya ndani ya chumba alichokuwa Stacie ikaanza kuita, iliita na kuita lakini haikupokelewa kitu kilichoonekana kuwashangaza sana. Hawakutaka kukubali, wakampigia simu meneja wake, haraka sana, simu ikapokelewa.

    “Upo na Stacie?” aliuliza dada wa mapokezi baada ya salamu.

    “Hapana! Yupo chumbani kwake, kwa nini unauliza hivyo?” aliuliza Robert.

    “Tunampigia simu, hapokei, unaweza kumpigia kwani tunahitaji kumuhudumia,” alisema msichana huyo.

    “Hakuna tatizo, namfuata hukohuko chumbani,” alisema Robert na kukata simu.

    Akatoka chumbani humo na kwenda chumbani kwa Stacie kwa lengo la kuzungumza naye kwamba wahudumu walitaka kumhudumia, alipoufikia mlango, akagonga hodi, kama ilivyokuwa kwa wahudumu, naye ilitokea vilevile, hakukuwa na sauti yoyote iliyosikika kutoka ndani.

    “Stacie, fungua mlango,” alisema Robert lakini hakukuwa na majibu yoyote yale.

    Alichokifanya ni kuufungua mlango na kuingia ndani, taa zilikuwa zikiwaka, alipigwa na mshtuko mkubwa baada ya kuangalia kitandani na macho yake kutua kwa msichana Stacie aliyekuwa amefariki kitandani pale.

    Robert akachanganyikiwa, hakutaka kubaki chumbani humo, harakaharaka akatoka na kumpigia simu mbunifu wa mavazi, Alejandro na kumwambia kile kilichokuwa kimetokea.

    “Unasemaje?” aliuliza Alejandro huku akionekana kuchanganyikiwa.

    “Ndiyo hivyo! Ngoja nikatoe taarifa...”

    Robert alionekana kuchanganyikiwa, akatoka hapo na kwenda mapokezini huku akikimbia, hakuamini kile kilichokuwa kimetokea, kwake, ilionekana kama ndoto fulani hivi ambapo baada ya muda angeamka na kujikuta akiwa kitandani.

    Alipofika mapokezi, kila mtu akabaki akimwangalia, hawakujua sababu iliyomfanya kutoka chumbani kwake na kuja mahali hapo huku akionekana kuwa kwenye presha kubwa.

    “Kuna nini?”

    “Ninataka kuongea na uongozi,” alisema Robert, watu waliokuwa pembeni, nao wakamsogelea, walitaka kujua kuna nini.

    “Kuna nini kaka?”

    Hapo ndipo Robert alipoanza kuhadithia kile alichokutana nacho chumbani kwa Stacie, hawakuamini, walichokifanya wahudumu hao ni kwenda huko chumbani kuhakikisha.

    Kile walichoambiwa ndicho walichokutana nacho, msichana Stacie alikuwa kitandani, hakuwa akipumua, alikufa kwa kunyongwa lakini kwa jinsi ilivyoonekana, alionekana kama mtu aliyekuwa akijidunga madawa ya kulevya.

    “Alikuwa akijidunga!” alisema mhudumu mmoja.

    “Nashangaa! Sikuwahi kumuona akitumia madawa ya kulevya, si hivyo tu, hata kusikia tetesi sehemu yoyote ile,” alisema Robert.

    “Sasa imekuwaje leo atumie madawa ya kulevya?”

    “Hata mimi nashangaa.”

    Kwa kuwa hawakuwa na maneno yoyote yale, walichokifanya ni kumpigia simu meneja wa hoteli hiyo ambaye alifika na kushuhudia kile kilichokuwa kimetokea, hawakumpigia huyo tu, bali waliwapigia simu polisi ambao kwa haraka sana wakafika mahali hapo.

    Kile walichokiona hakikuwa kigeni katika macho yao, katika kipindi hicho, watu waliokufa hotelini walikufa kwa staili hiyohiyo na muuaji alikuwa mmoja tu, huyo alikuwa Benjamin.

    Polisi hawakutaka mwili huo uguswe, bado walitakiwa kuuchunguza na kugundua kifo chake kilisababishwa na nini. Kitendo cha wahudumu kugundua kwamba msichana Stacie alikuwa amekufa chumbani humo, taarifa hizo wakaanza kuzisambaza katika mitandao ya kijamii.

    Kila mtu aliyezipata, alishtuka, hawakuamini kile walichokiona kwamba msichana huyo alikuwa amekufa ndani ya chumba cha hoteli. Hawakutaka kujiuliza sana, wakajua kwamba muuaji alikuwa yuleyule aliyekuwa akitafutwa kila kona, Benjamin ambaye mpaka katika kipindi hicho hakukuwa na mtu aliyejua mahali alipokuwa.

    “Ila kwa nini anaua jamaniiii?” aliuliza msichana mmoja huku akiwa ameishika simu yake, kile alichokiona, hakukiamini hata kidogo.

    “Mimi mwenyewe nashangaa...halafu yeye anaua masupastaa wanaochipukia, kwa nini lakini?” alisema msichana mwingine.

    Ndivyo ilivyokuwa. Taarifa zile ziliendelea kusambaa kila kona, watu walilia kwani hakukuwa na msichana ambaye waliamini kwamba angefanikiwa na kuwa na mashabiki wengi kama Stacie kutokana na mvuto aliokuwa nao.

    Baada ya siku mbili mwili kuchunguzwa, taarifa zikasikika kwamba muuaji alikuwa yuleyule, mtu hatari aliyeogopwa, Benjamin ambapo kwa kipindi hicho, FBI waliamua kumtafuta kwa nguvu kubwa kwani pasipo kufanya hivyo, angeendelea kuua.

    ****

    “David! Umefikia wapi?” aliuliza Benjamin kwenye simu.

    “Kila kitu tayari, ushahidi upo wa kutosha, nikutumie kwenye barua pepe?’ aliuliza David.

    “Sawa. Nitumie, hata kama kuna sauti nitumie pia,” alisema Benjamin.

    “Hakuna tatizo. Ila unajua kwamba keshokutwa pia kuna mauaji yatafanyika?” aliuliza David.

    “Hapana! Imekuwaje tena?”

    “Huyu jamaa anataka kumuua mrembo wa dunia.”

    “Unasemaje?”

    “Ninavyoongea tayari kashatuma watu kwenda Las Vegas kwa ajili ya kufanikisha mpango huo,” alisema David.

    “Kwa hiyo atatumia alama zangu za vidole?”

    “Nadhani!”

    Benjamin akabaki kimya kwa muda, hakutaka kuendelea na mazungumzo hayo, hapohapo akakata simu. Alikuwa kwenye mawazo mengi, hapo alipokuwa, haikuwa sehemu sahihi ya yeye kuwepo kwani alihisi kwamba muda wowote ule angekamatwa.

    Alipanga kuondoka Boston na kuelekea New York, alitulia katika viti vya abiria katika kituo cha treni cha Smallville, alitaka kukimbilia huko kwani hapo Boston hakukuonekana kuwa salama katika maisha yake.

    Japokuwa kulikuwa na watu wengi kituoni hapo lakini hakukuwa hata na mmoja aliyekuwa amemgundua. Aliendelea kubaki hapo mpaka treni ilipofika, haraka haraka akasimama na kwenda kuingia ndani, akatafuta kiti na kutulia.

    Treni haikusimama sana kituoni hapo ikaanza safari ya kuelekea jijini New York.Humo ndani ya treni, hakutaka kumwangalia mtu yeyote yule, alikuwa kimya huku muda wote akiwa anaangalia chini na huku kofia ikiwa kichwani mwake.

    Wakati akiwa katika hali hiyo, ghafla akashtukia kuona wanaume wawili waliokuwa wamevalia suti wamesimama mbele yake, harakaharaka akayainua macho yake na kuwaangalia watu hao, hawakuzungumza kitu, walibaki wakimwangalia, walipomuona kama mtu aliyechanganyikiwa, wakatoa beji zao zilizoonyesha kwamba walikuwa maofisa wa FBI.

    “Upo chini ya ulinzi Benjamin. Hatutaki ulete fujo, tulia hivyohivyo,” alisema ofisa mmoja. Benjamin akatii. Wanaume hao wakakaa pembeni yake, mmoja upande wa kushoto na mwingine upande wa kulia.

    ****

    FBI walikuwa na kazi kubwa mbele yao, hawakujua ni kwa jinsi gani wangeweza kumpata Benjamin ambaye alionekana kuwa mtu hatari sana, mtu ambaye hakutaka kuachwa akitanua mitaani hata mara moja.

    Mauaji mengi yalitokea, yaliitetemesha Marekani na duniani kote kwa kuwa hao waliouawa walikuwa watu maarufu sana, watu waliofanikiwa kuiteka mioyo ya watu wengi duniani.

    Walikesha usiku na mchana, walitegesha kamera sehemu nyingi hasa katika Jiji la Boston ambapo huko ndipo waliamini Benjamin alikuwepo katika kipindi hicho.

    Watu waliopewa kazi ya kumfuatilia usiku na mchana hawakutakiwa kulala hata mara moja, walipewa agizo kwamba walitakiwa kuhakikisha kamera zinafanya kazi kila saa na kila kitu kitakachokuwa kikiendelea kiwe kinarekodiwa.

    Hilo halikuwa tatizo, watu wa IT kutoka katika shirika hilo la kijasusi wakawa wanafanya kazi zao kama vile walivyoagizwa. Siku ziliendelea kukatika mpaka walipofanikiwa kumuona mtu aliyefanana na Benjamin akiingia katika Kituo cha Treni cha SmallVile.

    Kitu cha kwanza walichokifanya ni kuivuta picha yake kwa karibu, hakuwa akionekana vizuri lakini kingine walichokifanya ni kuichukua picha yake nyingine ambayo alikuwa akionekana usoni na kisha kuilinganisha na picha ile.

    Kila kitu kilifanana, kompyuta ikaandika neno 100 Match yaani ikimaanisha kwamba kila kitu kilikuwa sawa kati ya ile picha ya kichwa na picha ie ambayo ilipigwa katika kituo cha treni.

    Walichokifanya ni kuwasiliana na maofisa wa FBI na kuwaambia kile kilichokuwa kimetokea, harakaharaka wakawaagiza watu kuelekea huko huku wakiwatumia picha jinsi alivyovaa ili asiweze kuwapotea.

    Hilo halikuwa na tatizo, wakaondoka kuelekea huko. Walikuwa maofisa wawili waliokuwa na bunduki, kama kawaida yao walivalia suti nyeusi. Walikwenda mpaka walipofika katika kituo hicho cha treni.

    Haikuwa kwenda na kumuona bali walitakiwa kumtafuta na kuona alikuwa wapi, hivyo ndivyo walivyofanya, wakajifanya kuwa bize, waligawana kila mtu kuwa kivyake, kwa bahati nzuri wakati treni imefika, wakafanikiwa kumuona akisimama harakaharaka kuifuata treni, akaingia ndani na safari kuanza.

    ****

    Muda wote msichana Vivian alikuwa akilia tu, hakuamini kama mwisho wa siku angekamatwa na kuingizwa ndani ya chumba hicho kilichokuwa na giza totoro. Alipiga kelele kuhitaji msaada wa kutolewa ndani ya chumba hicho lakini hakukuwa na mtu aliyejali, hata mtu wa kuufungua mlango huo hakutokea kabisa, bado chumba kilikuwa kimefungwa.

    Saa zilisogea, alipoona amepiga sana kelele pasipo kupata msaada wowote ule akaamua kubaki kimya na kuona ni kitu gani ambacho kingeendelea. Baada ya kukaa ndani ya chumba hicho kwa saa kadhaa, mlango ukafungiliwa, mwanaume mmoja aliyekuwa na tochi akaingia na kummulika tochi usoni, mkononi alikuwa ameshika sahani iliyokuwa na chakula, alichokifanya ni kumrushia pale alipokuwa.

    “Please let me out of here,” (Naomba unitoe hapa, tafadhali) alisema Vivian huku akilia.

    “We can’t let you out of here, you have ten minutes to eat your damn food,” (hatuwezi kukutoa hapa, una dakika kumi za kula chakula chako) alisema mwanaume yule kisha kuufunga mlango.

    Vivian akaanza kutambaa pale sakafuni, aliona wakati sahani ikisukumwa kule alipokuwa hivyo alitambaa kwa hisia kwamba sahani ilikuwa sehemu fulani. Hiyo ilimfanya kuwa rahisi sana kuipata sahani hiyo ambapo akaichukua na kuanza kula.

    Alikuwa kwa kuwa alikuwa na njaa lakini hakuona radha yoyote ya chakula hicho, alitumia dakika saba tu kula, alipomaliza, akajisogeza pembeni na kuanza kulia tena.

    Hakuona kama angeweza kutoka ndani ya chumba hicho, watu waliokuwa wamemkamata, hawakumtaka yeye, wao walimtaka Benjamin ambapo hakujua kama kulikuwa na kosa lolote alilolifanya mpenzi wake mpaka watu hao kumtafuta na kutaka kumuua kwa gharama zozote zile.

    Alitamani kuwapigia simu watu wake wa karibu na kuwapa taarifa lakini alishindwa kufanya hivyo kwani kipindi alichokuwa ametekwa, hakuwa na simu yoyote ile, alifikishwa humo ndani akiwa mikono mitupu.

    Alichokifanya ni kumuomba Mungu kwani hakukuwa na njia nyingine ambayo ingemuwezesha kutoka ndani ya chumba hicho kwani hao watu waliomkamata, walionekana kutokuwa na masihara hata kidogo.



    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Wewe ni muuaji,” alisema polisi mmoja aliyekuwa na koti lililoandikwa BPD yaani Boston Police Department.

    “Hapana! Mimi si muuaji,” alisema Benjamin huku akimwangalia mwanaume huyo usoni, hakuwa peke yake, alikuwa na wanaume wengine, wote walikuwa polisi.

    Walimkamata Benjamin kwa kuwa walihisi kwamba yeye ndiye aliyekuwa akifanya mauaji ya watu wote waliokuwa wameuawa vyumbani mwao, walikuwa na uhakika kwa sababu alama za vidole vyake zilikutwa katika miili ya maiti hizo na baadhi ya vitu ndani ya chumba hicho.

    Benjamin alikuwa akilia huku akiendelea kujitetea kwamba hakuwa muuaji, hakuwahi kuua kama dunia ilivyokuwa ikijua bali kulikuwa na mtu nyuma ya kila kitu kilichokuwa kikiendelea.

    Kukamatwa kwake ilikuwa siri kubwa, hakupewa mwandishi wa habari yeyote yule, waliwaacha Wamarekani waendelee kuwalaumu lakini walitaka kufanya vitu vyao kwa mpangilio kwani kama taarifa zingetoka na kusema kwamba walimkamata Benjamin, wangeweza kuharibu kila kitu.

    “Tunajua kwamba hujafanya mauaji Benjamin japokuwa alama za vidole vyako zimekutwa katika maiti zilizokuwa katika vyumba,” alisema polisi mmoja.

    “Kweli sijafanya mauaji.”

    “Sawa! Ila kama hukufanya, nani alifanya?” aliuliza mwanaume huyo.

    Hapo ndipo Benjamin akaanza kusimulia kila kitu kilichotokea tangu siku ya kwanza alipopigiwa simu na Bwana Seppy na kuambiwa kazi kubwa ya kufanya mauaji iliyokuwa mbele yake, aliwaambia wazi kwamba alikataa hivyo kumteka yeye na mpenzi wake, wakamtisha lakini pamoja na hayo yote, alikataa kufanya mauaji hayo.

    “Ikawaje?”

    “Walinipa simu ya iPhone, nilipoishika, nafikiri ndipo walipata alama za vidole vyangu ambazo wamekuwa wakiziweka kila kona,” alisema Benjamin.

    “Una chochote cha kushikilia dhidi ya Bwana Seppy?’ aliuliza polisi mmoja.

    “Ndiyo! Nina rafiki yangu ambaye amekuwa akizifuatilia meseji na simu za mzee huyu kila kitu kilichokuwa kikiendelea, kwa maana hiyo ushahidi upo wote,” alisema Benjamin.

    Polisi wale hawakutaka kuzungumza kitu chochote, walitaka kufahamu kama kulikuwa na ushahidi kwani kumfikisha mahakamani mtu mzito kama Bwana Seppy haikuwa rahisi, ilikuwa ni lazima ujikamilishe kwa kila kitu.

    Mara baada ya kukata walichokitaka, hapohapo polisi hao wakatoka ndani ya chumba kile. Benjamin akabaki kimya, kichwa chake kilikuwa na mawazo tele, hakuamini kile kilichokuwa kikiendelea katika maisha yake.

    Hapo ndipo mawazo juu ya mpenzi wake, Vivian yalipomjia kichwani mwake, hakujua alikuwa wapi baada ya kutekwa, kabla ya kufanya kitu chochote ilikuwa ni lazima ajue mahali alipokuwa.

    Wakati akiwa kwenye mawazo lukuki, hapohapo mlango ukafunguliwa na wanaume wawili waliokuwa na makoti yaliyosomeka FBI wakaingia na kukaa katika viti vilivyokuwa chumbani humo.

    Mwanaume wa kwanza alijitambulisha kwa jina la Brett Phillip na mwingine Ryan Cashman. Watu hao walifika mahali hapo kwa kuwa walitaka kumuhoji maswali kadhaa juu ya kile kilichokuwa kimetokea.

    “Sikuwahi kuua, nililazimishwa kufanya hivyo ila nikakataa,” alisema Benjamin huku akiwaangalia wanaume hao usoni, tena kwa zamu.

    “Kama hukuua, nani aliua?” aliuliza Brett.

    Kama alivyowaambia polisi wale ndivyo alivyowaambia hata maofisa hao wa FBI kwamba hakuhusika katika mauaji hayo bali kulikuwa na mtu mwingine ambaye ni bilionea ndiye aliyehusika katika mauaji yote yaliyotokea.

    “Bwana Seppy! Haiwezekani,” alisema Brett.

    “Ndiyo hivyo! Ushahidi upo tayari, kama hamuamini, natumaini kuna siku mtaamini, hasa tutakapokwenda mahakamani,” alisema Benjamin.

    ****

    Taarifa za ndani kabisa zilisema kwamba yule muuaji aliyekuwa akitafutwa kwa udi na uvumba, Benjamin alikuwa amekamatwa jijini Boston na hivyo kushikiliwa na polisi.

    Kila aliyezisikia taarifa zile, hakuamini masikio yake kama kweli muuaji huyo aliyekuwa akichukiwa kila kona alikuwa amekamatwa na polisi. Taarifa hizo zilisambaa kwa kasi kubwa kama moto wa kifuu, kwenye mitandao ya kijamii, taarifa hizo zilisambazwa kila kona kiasi kwamba watu wengine wakahisi kwamba hazikuwa na ukweli wowote ule.

    Hapo ndipo watu walipoamua kutaka kumuona huyo Benjamin. Wengi wakahisi kwamba zilikuwa taarifa za uongo ambazo zilitengenezwa na polisi ili waweze kujisafisha kutokana na uchafu waliokuwa nao wa kushindwa kumtafuta Benjamin na kumkamata.

    Polisi hawakutaka kuzungumzia lolote lile, walikuwa na msemaji ambaye yeye ndiye aliyehusika kutoa taarifa kwa wananchi, kwa kuwa taarifa hizo zilivuja, hawakutaka kuthibitisha juu ya hilo.

    Baada ya taarifa hizo kusambaa kila kona, siku mbili baadaye ndipo polisi walipothibitisha kukamatwa kwa Benjamin na hivyo kuwaambia wananchi kwamba mua wowote ule kuanzia kipindi hicho angefikishwa mahakamani kusomewa mashitaka kwa kile alichokuwa amekifanya.

    Hicho ndicho kilichokuwa kikisubiriwa kwa hamu kubwa, watu wakaandaa mabango yao na kuandika jumbe nzito kwamba mahakama isilete masihara katika kesi hiyo, ilikuwa ni lazima kumhukumu Benjamin kwa kosa la mauaji kwa kile alichokuwa amekifanya.

    “Just hung him,” (Mnyonge) liliandikwa bango moja.

    Watu hawakuishia kuandika mabango hayo tu bali siku iliyofuata wakaanza kuandamana kuitaka mahakama imuhukumu kifo Benjamin kwa kile kilichotokea.

    Muda wote wakati hayo yakiendelea, Benjamin alikuwa sero, huko hakutakiwa kuzungumza na mtu yeyote yule, alitakiwa kukaa hivyohivyo mpaka pale kesi ingeanza kusikilizwa.

    Mtu pekee aliyeruhisiwa kuingia na kuzungumza naye alikuwa mwanasheria wake ambaye alimhadithia kila kitu kilichokuwa kimetokea na kwamba hakuhusika katika mauaji hayo yaliyokuwa yametokea.

    “Kwa hiyo unamaanisha Bwana Seppy ndiye aliyefanya mauaji?” aliuliza mwanasheria wake, Bwana Donald Gilphin.

    “Ndiyo! Ushahidi upo wa mawasiliano yake aliyokuwa akiyafanya,” alisema Benjamin.

    “Kama yapo, hakuna tatizo, hapo ndipo ninapopataka,” alisema mwanasheria.

    Mitaani hakukukalika hata mara moja, kila kona, watu walikuwa wakiandama huku wakiishinikiza mahakama kumuhukumu kifo Benjamin kwa kile kilichokuwa kimetokea kwa kuua watu wengi ambao walitabiriwa kuwa mastaa wakubwa hapo baadaye.

    Maandamano hayo yalikusanya watu wengi, si hapo Boston tu bali katika sehemu mbalimbali nchini Marekani watu walizidi kuandamana kila siku. Kama kuanza, walianza hapo Boston, wakaitikia Texas, New Orleans, New York, Washington na sehemu nyingine nyingi, kote huko walitaka kushuhudia Benjamin akihukumiwa kifo tu.

    Siku ziliendelea kukatika, baada ya siku kadhaa, Benjamin akachukuliwa na kufikishwa mahakamani. Siku hiyo ilikuwa ni hatari mitaani, watu walikuwa na mabango yaliyoitaka mahakama imuhukumu kifo Benjamin kwa kile kilichokuwa kimetokea.

    Moyo wake uliumia sana kwani alijua kwamba hakuua na wala hakuwahi kuua lakini hilo watu hawakulielewa, alitamani sana kuwaambia watu wote ukweli juu ya kilichokuwa kimetokea lakini hakupata muda huo, hasa siku ya kwanza kusikiliza kesi.

    Siku hiyo, alisomewa mashitaka tu na kisha kesi yake kupangwa kusikilizwa baada ya wiki mbili, baada ya hapo alitakiwa kuwasubiri watu wengine na kisha safari ya kuelekea rumande kuanza. Pale alipokuwa, hakuwa na amani kabisa, watu walitaka kuona akihukumiwa kifo tu na si vinginevyo.

    Waandishi wa habari hawakuwa nyuma, wakati yeye na watu wengine wakipelekwa katika basi kubwa la gereza, wakaanza kupiga picha kwani kwa kipindi hicho, Benjamin alikuwa biashara kubwa sana mitaani.

    “I hate him...” (ninamchukia) alisikika mwanamke mmoja aliyekuwa mahakamani hapo.

    “I hate him too, he is not supposed to live,” (hata mimi namchukia, hastahili kuishi) alisikika mwanamke mwingine.

    Hicho ndicho kilichokuwa ndani ya mioyo ya Wamarekani, hawakumpenda kabisa Benjamin, walimchukia kwa kuwa waliamini kwamba yeye ndiye aliyehusika katika mauaji yote yaliyokuwa yametokea.

    Moyo wake haukuacha kuuma, kila siku maumivu yalikuwa ni sehemu ya maisha yake. Kwa sababu kitu kilichokuwa kikisubiriwa ni kujitetea mahakamani kutokana na yale yaliyokuwa yametokea, hivyo wazazi wake na baadhi ya ndugu zake wakaruhusiwa kuzungumza naye tena huku akiwa chini ya ulinzi mkali.

    “Ni kweli uliua mwanangu?’ aliuliza baba yake.

    “Hapana baba! Sijaua, niliambiwa niue lakini nikakataa.”

    “Nani alikwambia?”

    “Bwana Seppy! Sijajua kwa nini alitaka kuua kipindi hicho ila yeye ndiye aliyehusika katika mauaji yote na kuacha alama za vidole vyangu,” alijitetea Benjamin.

    “Ilikuwaje hapo?”

    Hapo ndipo Benjamin alipoanza kuhadithia kila kitu, hakutaka kuficha kitu chochote kile kwani aliamini kupitia wazazi wake na baadhi ya ndugu waliokuwepo hapo alipokuwa wangeweza kuibadilisha mioyo ya watu wote duniani ambao walikuwa wakiamini kwamba aliua kumbe hakufanya hivyo.

    “Nitasimama kidete mpaka kijana wenu ashinde, hii kesi haina nguvu tena,” alisema mwanasheria wake ambaye naye alisimama kama wakili wake, Donald.

    Siku ziliendelea kukatika mpaka ilipofika siku ya kupandishwa tena mahakamani. Kama kawaida watu wengi walikusanyika mahakamani hapo, walitaka kushuhudia kile ambacho kingeendelea na Benjamin angejitetea vipi juu ya yale mauaji aliyokuwa ameyafanya.

    Wakati akiingia mahakamani, watu walianza kuzomea, hawakutaka kabisa kumuona katika uso wa dunia, walitaka kuona akihukumiwa kifo kwani hata kama angefungwa kifungo cha maisha gerezani bado watu wasingeridhika kabisa kutokana na mauaji aliyokuwa ameyafanya.

    Maofisa wa FBI walikuwepo mahakamani hapo, walikuwa wakifuatilia kila kitu, waliufahamu ukweli uliokuwa umejificha, walimwangalia Benjamin, walimuonea huruma kwani hakuwa ameua kama dunia ilivyokuwa ikiamini.

    Baada ya dakika kadhaa, hakimu ambaye alitakiwa kusikiliza kesi hiyo akaanza kuingia ndani ya mahakama hiyo, watu wote waliokuwa humo ndani wakasimama kama kumpa heshima, walipomwangalia, wakagundua kwamba alikuwa McRegan, miongonimwa mahakimu waliokuwa na rekodi kubwa ya kuwahukumu watu vifo.

    Kidogo mioyo yao ikaridhika, kitendo cha kumuona McRegan akiingia mioyo yao ilikuwa na furaha tele kwa kuona kwamba hatimaye kilio chao kilisikika na mambo yangekwenda vizuri kabisa kama walivyotaka iwe mioyoni mwao.

    Baada ya hakimu kukaa, watu wote hapo mahakamani wakakaa na kuanza kusikiliza. Kesi kwanza ikaanza kusikilizwa kwa muda kisha kupewa nafasi upande wa mshtaki ambaye ni Jamhuri ya Marekani, wakili wake, Bwana Peters akasimama na kuanza kumuuliza maswali Benjamin.

    “Bila shaka unaitwa Benjamin Saunders,” alisema Peters.

    “Ndiyo mheshimiwa.”

    “Unajua kwa nini upo hapa?”

    “Ndiyo mheshimiwa.”

    “Upo hapa kwa kosa la mauaji, ni kweli?”

    “Ni kweli mheshimiwa.”

    “Ni kweli uliua?”

    “Hapana!”

    “Sasa kama hukuua, kwa nini upo hapa?”

    “Kwa sababu nimesingiziwa kuua.”

    “Ila alama za vidole vyako vilikutwa katika kila mwili wa marehemu, unalizungumziaje hilo? Tuna majibu ya vipimo vyote, picha zako zilibandikwa kila kona, kila mtu anajua kwamba wewe ni muuaji, unakataa pia?’ aliuliza Peters.

    “Ndiyo mheshimiwa. Ninakataa kwa sababu sikuua!”

    “Kama kweli hukuua, kwa nini ulikuwa uunajificha baada ya kugundua kwamba unatafutwa?” aliuliza Peters.

    “Nilikuwa najificha si kwa sababu niliua, ila nilikuwa najificha kwa sababu nilitakiwa kuuawa muda wowote ule,” alisema Benjamin.

    “Ulitakiwa kuuawa! Na nani?”

    “Bwana Seppy, huyu bilionea,” alijibu Benjamin, minong’ono ikaanza kusikika humo mahakamani.

    “Kwa nini alitaka kukuua?”

    “Kwa sababu nilikataa kuua.”

    “Kumuua nani?”

    “Wote nilioambiwa kwamba nimeua.”

    “Kivipi?”

    Hiyo ndiyo ilikuwa nafasi yake, hakutaka kuchelewa, akaanza kuhadithia kila kitu kilichotokea katika maisha yake, alianzia tangu siku ya kwanza kabisa alipopigiwa siku wakati alipokuwa jijini Washington, kipindi ambacho yeye na Wamarekani wengine walitaka kumsikiliza rais katika hotuba ambayo alitakiwa kuitoa katika siku hiyo ya uhuru wa Marekani.

    Hakuishia hapo, alizungumzia namna alivyopigiwa simu na mtu asiyemfahamu ambaye alimtaka kuonana naye sehemu fulani, alitii kwani kama asingefanya hivyo mpenzi wake angeuawa.

    Ilikuwa ni simulizi iliyochukua zaidi ya dakika ishirini, mahakama ilikuwa kimya ikimsikiliza. Alisimulia huku akionekana kuumizwa sana na muda wote alikuwa akilia tu.

    Aliiambia mahakama kwamba hakuua bali Bwana Seppy ndiye aliyeua na hata alama za vidole vyake zilitengenezwa baada ya kupewa simu ya iPhone kwa ajili ya mawasiliano, kitendo cha kuishika simu ile tu, akawa ameacha alama za vidole vyake.

    “Mheshimiwa hakimu, kwa mamlaka ya mahakama, naomba Bwana Seppy akamatwe na kufikishwa mahakamani kwani tumegundua kwamba mteja wetu hana hatia,” aliingilia wakili wake, Bwana Donald japokuwa haikuwa ikiruhusiwa.

    Hakimu hakuwa na cha kufanya zaidi ya kutoa amri Bwana Seppy afikishwe mahakamani kwani kwenye kesi ile na yeye alitajwa kama mhusika katika mauaji yale. Mahakama ikawa kimya, mpaka katika kipindi ambacho Benjamin alikuwa akishuka kizimbani, watu walibaki wakimwangalia kwa huruma kubwa.

    Kila kitu kikabadilika, chuki walizokuwa nazo watu dhidi yake zikaanza kupotea mioyoni mwao baada ya kugundua kwamba hakuwa muuaji bali aliambiwa aue lakini akakataa na hivyo ujanja kufanyika kwa ajili ya kumuingiza matatani.

    “Hii kesi utashinda. Ila ushahidi unao?” aliuliza Bwana Donald.

    “Upo! Ni lazima tumtafute David, ana ushahidi wote, kama hatutompata, tutashindwa,” alisema Benjamin.

    “Basi sawa. Nitawasiliana na polisi ili waweze kuwasiliana naye, baada ya wiki mbili, ushahidi uwe tayari,” alisema Donald.

    “Nitashukuru.

    ****http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Bwana Seppy alikuwa akifuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea, Dracula aliyekuwa mahakamani kazi yake kubwa ilikuwa ni kumtumia ujumbe mfupi juu ya kila kitu kilichokuwa kikijiri huko.

    Moyo wake ulikuwa na hofu kubwa baada ya Benjamin kupinga kufanya mauaji hayo na mwisho wa siku kulitaja jina lake. Aliiona dunia ikiwa imemuangukia, kila mtu mbele yake alikuwa akimzomea na mbaya zaidi aliiona milango ya gerezani ikifunga na yeye kuchukuliwa na kuingizwa humo.

    Alisikitika mno, alijuta na wakati mwingine alikuwa akijiulaumu juu ya sababu iliyomfanya kufanya mauaji yale na wakati alikuwa na uwezo wa kukaa kimya na maisha kuendelea kama kawaida.

    Siku hiyohiyo akafuatwa na maofisa wa FBI ambao walimtaka kuondoka naye kutoka hapo New York alipokuwa akiishi na kuelekea jijini Boston. Alijifanya kutokujua kitu chochote kile, wakamwambia kwamba angepewa taarifa juu ya kilichokuwa kikiendelea mara baada ya kufika katika kituo cha polisi.

    Kipindi hicho polisi hawakuhusika, walijua kwamba mtu huyo alikuwa na jina kubwa hivyo ingekuwa rahisi kwake kutengeneza watu wake katika vituo mbalimbali vya polisi na ndiyo maana hata kwenye kumkamata, walikwenda maofisa wa FBI na si polisi kama ilivyotakiwa iwe.

    “Benjamin amekutaja kwamba umehusika katika mauaji, ni kweli?” aliuliza ofisa wa FBI huku wakiwa wamemuweka ndani ya chumba kilichokuwa na kioo katika upande mmoja wa ukuta, hakujibu kitu, akabaki kimya.

    “Kuna ukweli?” ofisa huyo akauliza tena swali.

    “Siwezi kuzungumza kitu chochote kile, namtaka mwanasheria wangu awe hapa,” alisema Bwana Seppy.

    Hilo halikuwa tatizo, walichokifanya ni kumpa simu yake na kumwambia awasiliane na mwanasheria wake ambaye ndani ya dakika ishirini, alikuwa katika kituo hicho.

    Alitajwa na mtuhumiwa wa mauaji kwamba yeye ndiye aliyehusika katika mauaji hayo, hivyo alitakiwa kujipanga kwani naye angepanda mahakamani na kujibu kesi iliyokuwa ikimkabili.

    “Unaona kama tunaweza kushinda kesi hii?” aliuliza Bwana Seppy, yeye mwenyewe alikuwa na hofu.

    “Kesi tunaweza kushinda kama huo ushahidi hautoweza kupatikana mahakamani,” alijibu mwanasheria wake ambaye angemfanya kuwa wakili wake hapo baadaye.

    “Kwa hiyo huo ushahidi inabidi upotee?”

    “Ndiyo hivyo!”

    Hilo halikuwa tatizo, kwa sababu Benjamin alisema kwamba kulikuwa na ushahidi, Dracula na wenzake wakaanza kufuatilia na mwisho wa siku kujua kwamba kulikuwa na mtu ambaye alifahamu kila kitu na ndiye ambaye alikuwa na ushahidi, huyu alikuwa David Belshaaz, mmoja wa marafiki wa Benjamin aliyekuwa akiishi hapo Boston na alikuwa akisomea masomo ya kompyuta katika Chuo cha Harvard.

    “Inabidi mmuue haraka iwezekanavyo,” alisema Bwana Seppy.

    “Hakuna tatizo.”

    Alichokifanya Dracula ni kuwatuma vijana wake waelekee katika Chuo Kikuu cha Harvard kwa ajili ya kumtafuta huyo David. Vijana hao hawakutaka kupoteza muda, harakaharaka wakaondoka kuelekea huko chuo ambapo baada ya kuulizia, wakaambiwa kwamba kijana huyo alikuwa akiishi West Mania, mtaa uliokuwa na wahuni wengi hapo Boston.







    Mbele yake, David aliiona hatari kubwa, alijua kwamba baada ya Benjamin kukamatwa na kujulikana kwamba yeye alikuwa na ushahidi wote kuhusu kile kilichokuwa kikiendelea basi angetafutwa tu.

    Alilijua hilo kwa kuwa kwenye kesi ile yeye ndiye alikuwa kila kitu, yaani yeye ndiye alikuwa na uwezo wa kumfunga Benjamin na yeye ndiye alikuwa na uwezo wa kumuweka huru kijana huyo.

    Aliyapenda maisha yake na hakutaka kabisa kuona akikamatwa na kufikishwa sehemu mbaya ambayo ingeyaweka maisha yake rehani na hata kuyapoteza kabisa.

    Alijipanga kwa kila kitu. Kila siku alihakikisha anaondoka nyumbani asubuhi na mapema kwenda maktaba, huko angekaa mpaka muda wa usiku wa manane ambapo angerudi nyumbani na kutulia, tena akiwa amejificha mpaka pale wiki mbili zingekatika na kutoa ushahidi wake mahakamani.

    Hiyo ndiyo ilikuwa ratiba yake ya kila siku. Kila siku alipokuwa akirudi usiku wa manane alikutana na hali ambayo alikuwa na uhakika kwamba kulikuwa na watu waliingia ndani kwake kutokana na mazingira aliyoyaacha, hayakuwa yale aliyoyakuta, akagundua kwamba kulikuwa na watu waliokuwa wakiingia.

    Wakati alipokuwa akirudi nyumbani, hakuwa akirudi kwa uwazi, alirudi kwa kificho sana kiasi kwamba hata majirani hawakuwa wakijua kama alikuwa akiishi ndani ya nyumba hiyo, na ilipofika asubuhi, kama kawaida yake aliondoka kisiri kuelekea maktaba kama kawaida yake.

    “Mambo...” alisikia sauti ya msichana ikimsalimia kwa sauti ya chini kabisa.

    David akageuka na macho yake kugongana na macho ya msichana mrembo mno, alipomwangalia, ilikuwa rahisi sana kusema kwamba msichana huyo alikuwa chotara, yaani alikuwa na mchanganyiko wa rangi, mzazi wake mmoja alikuwa mtu kutoka Brazil na mwingine alikuwa Mzungu.

    Kabla ya kuitikia salamu hiyo, David alibaki akimwangalia msichana huyo, mbali na uzuri wa sura aliokuwa nao, alikuwa na umbo zuri, alivutia na ngozi yake ilimdatisha kupita kawaida.

    “Poa..” aliitikia.

    “Kuna mtu hapa?” aliuliza msichana huyo.

    “Wapi? Hapo? Hakuna mtu, karibu,” alisema David huku akionekana kuweweseka.

    Hakukuwa na kusoma tena, kila wakati macho yake yalikuwa yakimwangalia msichana huyo kiwizi, alichanganyikiwa kutokana na uzuri aliokuwa nao, wakati mwingine alihisi kwamba alikutana na malaika kwa jinsi alivyokuwa na uzuri wa kuvutia.

    Alikuwa kama bubu, hakujua ni kitu gani alitakiwa kumwambia msichana huyo kwani ukweli ni kwamba alimpenda sana na asingeweza kumuacha kabisa, alijiuliza maswali mengi juu ya namna ya kumuingia msichana huyo mrembo.

    “Naitwa David Belshaaz,” alijitambulisha huku akimpa mkono.

    “Naitwa Veronica Twingle,” alijitambulisha msichana huyo kwa sauti ya chini ili wasiwasumbue watu wengine waliokuwa kwenye maktaba hiyo.

    “Unasoma wapi?”

    “Nasoma UCLA, nimekuja huku kwa ajili ya likizo fupi, wewe?” alijibu Veronica na kuuliza.

    “Ninasoma hapo Harvard.”

    “Waoo! Inaelekea una akili sana.”

    “Hapana! Nipo kawaida sana V.”

    “Mmh! Aya!”

    Hisia za kimapenzi zilimwendesha puta David, bado hakuamini kama alikuwa na msichana mrembo jirani yake. Mapigo yake ya moyo kila wakati yalidunda sana kuna wakati alitamani hata kumwambia Veronica waondoke hapo maktaba na waelekee sehemu, wazungumze sana.

    Muda ulizidi kwenda mbele, ilipofika majira ya saa kumi na moja jioni, David hakutaka kuendelea kuvumilia kwani kwa jinsi walivyokuwa wakipiga stori na kuzidi kuzoeana, aliona hiyo ndiyo nafasi ya kumwambia msichana huyo waondoke.

    “Tuondoke! Kwenda wapi?”

    “Sehemu yoyote nzuri! Hata hapo kwenye mbuga ndogo ya wanyama, unaonaje?’ aliuliza David, tabasamu halikumtoka usoni mwake.

    “Mmh!”

    “Nakuomba, ninahitaji sana kampani yako!”

    “Kuna usalama kweli?”

    “Ndiyo! Unahisi mimi ni mtekani?”

    “Hapana!”

    “Basi jua kuna usalama, na nitakulinda pia, amini kwamba upo katika mikono mikono salama,” alisema David kwa kujiamini.

    Kwa sababu aliahidiwa ulinzi, Veronica, msichana mpole hakuwa na jinsi, akakubaliana naye na hivyo kuondoka hapo maktaba na kuelekea huko alipotaka mwanaume huyo waelekee.

    Kwa kuwa yeye hakuwa na gari na msichana huyo alikuwa na gari lake, wakaingia na kuanza safari ya kuelekea huko walipokuwa wakielekea. Njia nzima David alikuwa akijichekesha tu, hakutaka kuonekana mkimya, alitaka kuonekana muongeaji sana ili aweze kumvutia msichana huyo na hatimaye auteke moyo wake.

    Veronica aliendesha gari mpaka pale geji ya mafuta ilipoanza kuonyesha kwamba gari hilo lilikuwa na mafuta kidogo hivyo walitakiwa kuongeza. Alichokifanya ni kutafuta kituo cha mafuta kwa ajili ya kulijaza mafuta gari hilo.

    Alipokiona, akakifuata kituo hicho, akateremka na kuushika mpira wa kujazia mafuta ndani ya gari kisha kuanza kujaza mafuta huku David akiwa ndani ya gari akimwangalia msichana huyo, kila alipomwangalia, alihisi kumpenda tu.

    Wakati akiwa amejisahau kumwangalia msichana huyo tena huku kioo kikiwa wazi kabisa, akashtukia akishikwa shati na mwanaume aliyekuwa nje ya gari, hata kabla hajaangalia alikuwa nani, akanusishwa kitambaa kilichokuwa na madawa ya usingizi, hapohapo, hakuchukua hata sekunde kumi, akaanza kuona giza machoni mwake, hakukuwa na alichokisikia zaidi ya sauti ya mwanaume ikimsifia msichana Veronica kwa kazi nzuri aliyoifanya, baada ya hapo, akapoteza fahamu.

    Veronica ambaye alikuwa akitabasamu tu aliwaangalia watu hao, aliwafahamu na ndiyo haohao waliomwambia kwamba aifanye kazi hiyo kwani huyo David alikuwa akihitajika sana.

    Akalipwa kiasi chake cha fedha, dola za kimarekani elfu ishirini na kisha wanaume hao kumchukua David, wakamuingiza ndani ya gari lao na kisha kuondoka naye mahali hapo.

    “Bosi alisema tumuue kupoteza ushahidi,” alisema jamaa mmoja.

    “Nakumbuka sana! Tutafanya hivyo tukifika katika jengo la mauaji,” alisema jamaa mwingine.

    “Haina noma.”

    ****

    Safari yao ilikuwa ikiendelea kama kawaida, kitu walichokuwa wakikihitaji kilikuwa ni kufanya mauaji tu. David alikuwa akilia, aliomba msamaha japokuwa hakujua ni mahali gani alikosea, alitaka kuachwa huru ili aondoke na si kuuawa kama watu hao walivyotaka.

    Hakuacha kulia, alifumbwa macho kwa kitambaa kizito, alihisi kwamba gari hilo lilikuwa safarini lakini hakujua lilikuwa likielekea mahali gani. Alichokiona mbele yake kilikuwa kifo tu, alitamani sana aachwe lakini hakukuwa na mtu aliyetaka kufanya kitu kama hicho.

    Safari iliendelea kwa dakika kama ishirini, katika safari nzima walikuwa wakizungumza kuhusu kumuua David kitu kilichomfanya kuogopa na kuona kwamba kama asingefanya juhudi zozote zile, watu wale wangeweza kumuua kama walivyotaka.

    “Tukishamuua, inakuwaje sasa?” aliuliza kijana mmoja.

    “Baada ya hapo, tumeambiwa tuutumbukize mwili wake ndani ya pipa la tindikali,” alijibu kijana mmoja.

    “Basi hakuna tatizo, kama ni hivyo, ipo poa,” alisema kijana huyo.

    Safari hiyo iliendelea mpaka gari hilo lilipofika katika jumba moja na kisha kuteremka pamoja na David ambaye bado alikuwa amefumbwa macho yake. Wakamchukua na kumpeleka ndani ya jumba hilo, hawakutaka kumuua haraka kama walivyoambiwa, iliwapasa kujipanga kwanza kwani mbali na huyo David, pia kulikuwa na msichana Vivian ambaye alitakiwa kushikiliwa mpaka pale watakapoambiwa nini cha kufanya juu yake.

    “Ingia humo kwanza,” alisema mwanaume mmoja, hapohapo akamsukuma David ndani ya chumba hicho ambapo humo ndani akatoa kitambaa kile kilichofumba macho yake, chumba kizima kilikuwa na giza.

    ****

    Kesi haikuonekana kuwa kubwa kwa upande wa Benjamin kwa kuwa kulikuwa na ushahidi ambao ulimhusisha Bwana Seppy kwamba alikuwa muuaji na ndiye yeye aliyepanga mauaji kwa watu wote waliokuwa wamekufa ambapo kulionyesha kwamba watu hao walijiua huku kukiwa na alama za vidole vya Benjamin.

    Mtu muhimu kwa kipindi hicho alikuwa David tu, ilikuwa ni lazima kumtafuta popote pale alipokuwa kwani baada ya wiki mbili mtu huyo alikuwa akihitajika mahakamani.

    Alielekezwa na Benjamin mahali alipokuwa akiishi David na kwenda huko lakini kitu cha ajabu kabisa kukutana nacho, nyumba ilikuwa imefungwa na hakukuwa na dalili kama kulikuwa na mtu humo ndani.

    Hilo lilimshtua sana, alitamani mno kwenda kuwauliza majirani lakini hilo halikuwezekana kwani katika mtaa huo, hakukuwa na watu waliokuwa wakionekana nje, wengi walikuwa ndani ya nyumba zao.

    Hakutaka kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kuondoka na huko alipokwenda alijaribu kumpigia simu David lakini kitu kilichomfanya kuwa na wasiwasi, simu haikuwa ikipatikana.

    Moyo wa Donald ukakosa amani, akahisi kwamba inawezekana kuwa kulikuwa na kitu kibaya kilitokea kwani Bwana Seppy alikuwa na mkono mrefu na alijua kwamba huyo David ndiye alikuwa mtu hatari hivyo kufanya kila linalowezekana kummaliza kabisa.

    Kwa kile kilichokuwa kimetokea, ilikuwa ni lazima kumpa taarifa Benjamin, hivyo akarudi na kumwambia kile alichokutana nacho. Kama ambavyo moyo wake ulivyokuwa na wasiwasi ndivyo ilivyokuwa hata kwa Benjamin.

    Haikuwa kawaida kwa David kuzima simu yake, muda mwingi simu yake ilikuwa hewani, sasa kwa nini siku kama hiyo azime simu yake tena msaa machache baada ya kusema kwamba alikuwa na ushahidi wa kutosha ambao ungemfanya Bwana Seppy kutiwa hatihani na hivyo kuhukumiwa kifo au kifungo cha maisha gerezani?

    “Nahisi kutakuwa na kitu,” alisema Benjamin huku akionekana kuwa na hofu.

    “Unahisi kwamba Bwana Seppy atakuwa amefanya kitu?” aliuliza Donald.

    “Nahisi hivyo, ni lazima atakuwa amefanya kitu,” alisema Benjamin huku akionekana kukata tamaa kwani pasipo David, inamaanisha kwamba yeye ndiye angehukumiwa kifo au kifungo cha maisha gerezani.

    Alichokifanya Benjamin ni kumwambia Donald kwamba ilikuwa ni lazima kuonana na maofisa wa FBI ili aweze kuwaambia kuhusu umuhimu wa David katika kesi hiyo.

    Hilo wala halikuwa tatizo, mara baada ya kupewa taarifa hiyo, maofisa wa FBI wakaanza kufanya mikakati yao ya kuhakikisha huyo David anapatikana kwani yeye ndiye alikuwa mtu muhimu kuliko wote katika kesi iliyokuwa ikimkabili Benjamin.

    Kitu cha kwanza kabisa kukifanya ni kwenda nyumbani kwake, kama ilivyomkuta Donald ndivyo ilivyowakuta hata wao, David hakuwepo na hawakujua alikuwa mahali gani.

    Mara ya kwanza wakahisi kwamba inawezekana alikuwa ndani amelala au ameuawa hivyo kufanya harakati za kuingia humo, walifanikiwa kupitia mlango wa nyuma, tena kwa kuvunja kioo na kutoa loki, wakaingilia jikoni, wakaangalia huku na kule, David hakuwepo.

    Hawakutaka kuishia hapo, wakaenda sehemu nyingine za nyumba hiyo ikiwemo chumbani mpaka bafuni na chooni, kama ilivyokuwa jikoni, napo majibu yalikuwa yaleyale, David hakuwepo kitu kilichowafanya kuhisi kwamba kulikuwa na watu kutoka kwa Bwana Seppy ambao walifika na kumteka kijana huyo, hivyo wakaanza kumtafuta kila kona, tena hasahasa walitumia kamera ndogo za mitaani, CCTV kwa kuamini kwamba wangepata kitu chochote kile ambacho kingewasaidia.

    ****

    Mitaani hali ya hewa ilibadilika, watu wote ambao waliitaka mahakama kumhukumu Benjamin kifo au kifungo cha maisha gerezani, wakabadilika na kumtaka mwanaume huyo huyo aachiwe huru na bilionea mkubwa duniani, Bwana Seppy apatikane haraka iwezekanavyo na kupandishwa kizimbani.

    Watu walilia mitaani, hawakuamini kile kilichokuwa kimetokea, maneno aliyosema Benjamin mahakamani kwamba yeye hakuhusika na mauaji bali Bwana Seppy ndiye alihusika yaliwafanya kupunguza chuki zao juu yake.

    Vichwa vyao vilichanganyikiwa, hawakujua ukweli ulikuwa wapi, hawakujua kama kweli Benjamin alikuwa amehusika au la, kitu walichokuwa wakikisubiria kilikuwa ni huyu shahidi ambaye alikuwa na ukweli wote ambao ungemuweka huru Benjamin.

    Baada ya saa kadhaa tangu Benjamin amtaje Bwana Seppy kama mhusika mkuu katika mauaji hayo, taarifa zilizoanza kusikika katika mitandao ya kijamii ni kwamba David, huyo shahidi aliyetarajiwa kumwaga kila kitu hadharani, hakuwa akionekana nyumbani kwake, alipotea katika mazingira ya kutatanisha kitu kilichowafanya watu kuona uwezekano kwamba mzee huyo bilionea alikuwa amehusika katika mauaji hayo.

    “Huyu mzee atakuwa amehusika...” alisema jamaa mmoja.

    “Kweli Bwana, haiwezekani baada ya kutajwa yeye, eti shahidi haonekani, hivi inawezekana hiyo?” alihoji jamaa mmoja.

    Hilo ndilo lililosikika mitaani, kila mtu alikuwa na uhakika kwamba Bwana Seppy ndiye aliyehusika katika mauaji ya watu wote waliouawa kinyama ndani ya hoteli.

    Mambo yaliendelea kubadilika na mwisho wa siku kila mtu akataka kitu kimoja tu, mzee huyo afikishwe mahakamani na kuhukumiwa kwa kile kilichokuwa kimetokea.

    Wenye mabango hawakutaka kusubiri, wakaondoka na kuelekea barabani, polisi walijitahidi kuwazuia lakini ilishindikana kabisa kwani kadiri muda ulivyokuwa ukienda mbele ndivyo walivyozidi kuongezeka mitaani na kuendelea kuitaka mahakama imhukumu kifo Bwana Seppy kwani kile alichokuwa amekifanya, hakika kiliiumiza mioyo yao.

    ****

    Vivian alikuwa chumbani mule, hakuweza kuona kitu chochote kile, aliletewa chakula kilichokuwa katika sahani lakini hakuwa na hamu ya kula, muda wote alikuwa mtu wa kulia tu, moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makali mno, hakuamini kama mwisho wa siku yeye ndiye angekuwa ndani ya chumba hicho ambapo mpaka hapo hakujua nini ingekuwa hatma yake.

    Aliendelea kulia huku akimfikiria mpenzi wake, hakujua alikuwa mahali gani na nini kiliendelea katika maisha yake. Alisikia huzuni kubwa moyoni mwake na wakati mwingine alipiga magoti na kumuomba Mungu japo amkomboe kutoka katika mikono ya watu hao ambao walionekana kuwa na lengo moja, kumuua.

    Siku ya kwanza ikapita pasipo kujua kwani ndani ya chumba kile kulikuwa na giza totoro ambalo lisingemfanya mtu yeyote kugundua kama ilikuwa wakati gani, siku iliyofuata, huku akiwa amechoka akapanga kuondoka ndani ya chumba hicho, hakujua angeondoka vipi lakini ilikuwa ni lazima kuondoka.

    Hapo ndipo alipoanza kupapasa huku na kule, alikuwa akitafuta upenyo wa kuondoka chumbani hapo. Kama zilivyokuwa nyumba nyingine nchini Marekani, hata nyumba ile, vyumba vyake vilikuwa vimetenganishwa kwa maboksi magumu hivyo akaona kwamba hiyo isingekuwa kazi kubwa kuondoka.

    Alichokifanya ni kuchukua viatu vyake vilivyokuwa na visigino virefu na kuanza kugonga kwenye boksi lililotenganisha chumba hicho na chumba kingine.

    Hakuwa na jinsi, ilikuwa kazi kubwa lakini ilimbidi kufanya hivyo kwani kama asingefanya hivyo, angeuawa mara tu watu wale waliomuweka ndani ya chumba hicho wangerudi kwa mara ya pili.

    Kugonga kwake hakukuacha, aliendelea kugonga zaidi na zaidi. Boksi lile lilikuwa kubwa lakini kutokana na kugonga kwa nguvu tena eneo moja pasipo kuacha, alama ikaanza kutoka katika boksi hilo.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hiyo ikampa nguvu ya kugonga zaidi, hakuacha, aliendelea kufanya hivyo zaidi na zaidi na mwisho wa siku akaona Mungu akiwa upande wake kwani boksi lile kubwa likaanza kuachia eneo kubwa, alipoendelea zaidi, chumba kikaacha kupenyezewa mwanga kupitia katika tundu lile lililopatikana.

    “Asante Mungu,” alijikuta akisema.

    Kabla ya kuendelea akaanza kuchungulia, alitaka kujua kama upande wa pili kulikuwa na watu wengine, alichungulia, sehemu ambayo alikuwa ametoboa ilikuwa katika chumba kingine, hakutaka kujiuliza kama kulikuwa na watu wengine ndani ya nyumba hiyo, jibu alilokuwa nalo ni kwamba ndani hakukuwa na mtu kwani kama kungekuwa na mtu, ni lazima angefika katika chumba kile kutokana na kuligonga boksi kwa kipindi kirefu.

    Aliendelea zaidi mpaka alipopata tundu kubwa na hatimaye kutoka ndani ya chumba kile. Moja kwa moja akaelekea katika chumba kile ambacho kilitenganishwa kwa ukuta wa boksi, akaufuata mlango na kuufungua.

    Kitu cha kwanza kabisa alichotaka kujua ni muda. Akatoka ndani ya chumba hicho na kuelekea sebuleni, nyumba nzima ilikuwa kimya na hakukuwa na dalili za kuwepo kwa mtu yeyote ndani ya chumba hicho.

    Alipofika huko, saa kubwa ya ukutani ilionyesha kwamba ni saa kumi na moja jioni, hakujali sana, akaufuata mlango na kutaka kuufungua kwa ajili ya kutoka ndani ya chumba hicho.

    “Mbona haufunguki...” alijisemea huku akiendelea kuufungua mlango huo.

    Mlango ulifungwa kwa ufunguo kwa nje, alijitahidi kuufungua lakini haukufunguka kabisa. Moyo wake ulikuwa ukidunda kwa nguvu, alichokuwa akikitaka ni kutoka katika nyumba hiyo tu kwani haikuwa sehemu salama hata mara moja.

    Alipoona mlango haufunguki, akatoka mlangoni na kuelekea katika vioo vya dirisha, vyote vilifungwa, alijaribu kuvunja vioo hivyo lakini ilishindikana, vioo vilikuwa vile vigumu ambavyo isingewezekana hata mara moja kuvunjika.

    “Nifanye nini?” alijiuliza.

    Hakutaka kuishia hapo, ilikuwa ni lazima ahakikishe anatoka ndani ya jumba hilo kubwa, akaondoka na kuelekea katika vyumba vingine, kama ilivyokuwa kule sebuleni ndivyo ilivyokuwa huko, alishangaa ni kwa jinsi gani nyumba hiyo ilikuwa na ulinzi mkubwa kiasi hicho.

    Alipita katika vyumba vyote isipokuwa chumba kimoja ambacho kilikuwa kigumu kufunguka. Hicho ndicho chumba alichohisi kwamba kulikuwa na njia nyepesi ya kutokea hivyo ilikuwa ni lazima kuingia ndani ya chumba hicho.

    Alijaribu na kujaribu kuufungua mlango huo lakini haukufunguka, aliendelea kujaribu zaidi na zaidi na baada ya dakika thelathini, mlango ukafunguka na hapohapo kuingia ndani.

    Alichokikuta hakuamini. Chumba kilikuwa na kiti kimoja kilichokuwa na kamba nyingi, pembeni kulikuwa na mkia wa taa uliokuwa ukitumika kuwachapa watu waliokuwa wakiingizwa ndani ya chumba hicho.

    Mbali na vito hivyo, pia kulikuwa na waya mmoja mkubwa uliogawanyika pande mbili, waya wa kuchajia betri za gari ambao ulitumika kama kuwatisha watu kwa kuwapiga shoti ya umeme.

    Mbali na hivyo, pia kulikuwa na kiti kidogo chini ambacho kilionekana kama kistuli kilichokuwa na tundu kwa chini sehemu ya kukalia. Hicho kilikuwa maalumu kwa kumkalisha mateka akiwa mtupu kisha kuanza kuzipiga korodani zake.

    Hicho kilikuwa chumba cha kutisha ambacho pia hata kuta zake zilionekana kuwa na michirizi ya damu zilizokuwa mpaka chini kabisa. Picha hiyo ilimtisha mno, hakutaka kubaki humo kwani hata harufu ya damu ilimghasi puani mwake, harakaharaka akatoka chumbani humo na kuelekea sebuleni.

    Macho yake yakatua katika simu ya mezani, hatakaharaka akaifuata ili aweze kuitumia kuwapigia polisi, alipouchukua mkonga wa simu na kupiga, hakuukuwa na sauti yoyote iliyosikika na alipoangalia, akakuta waya ukiwa umekatwa.

    Alichanganyikiwa, kila kitu alichotaka kukifanya ndani ya chumba hicho kilionekana kumbana sana. Muda ulikuwa umekwenda sana, saa tano zilikatika huku akiwa hapo sebuleni na saa ya ukutani ilionyesha kwamba ni saa nne usiku.

    Wakati akiwa anajifikiria zaidi nini cha kufanya, ghafla akasikia muungurumo wa gari kutoka nje ya nyumba hiyo, harakaharaka akazima taa na kuchungulia dirishani.

    Geti likafunguliwa na wanaume watatu wakatoka kutoka garini huku wakiwa na mwanaume mwingine ambaye walimfunga kitambaa machoni. Vivian hakujua mtu aliyekuwa ametekwa alikuwa nani, alichokifanya ni kwenda jikoni na kujificha huko.

    ****

    Wanaume wale baada ya kuingia ndani ya nyumba hiyo, wakampeleka David katika chumba kingine kabisa kilichokuwa na giza nene kama kile chumba alichowekwa Vivian. Wakamwambia akae huko kwani kulikuwa na kazi kubwa ya kutaka kufanya.

    Walichokifanya ni kutoka na kuelekea sebuleni, walisahau kabisa kuhusu msichana Vivian, walichokikumbuka ni kwamba walikuwa na jukumu dogo la kumuua David kama waliyoambiwa na bosi wao.

    “Let’s eat,” (tuleni kwanza) alisema mwanaume mmoja.

    Chakula kilikuwa kingi katika friji kiasi kwamba hawakuona dalili zozote kama kulikuwa na chakula kingine kilichokuwa kimechukuliwa na Vivian. Wakachukua na kukiweka mezani ambapo wakaanza kula huku wakiyafurahia maisha kwamba baada ya dakika kadhaa wangekwenda kuwa na fedha nyingi kutokana na malipo ambayo Bwana Seppy angeyafanya.

    “I will have my own Ferrari motherfu...” (nitakuwa na Ferrari yangu...)

    “Hahaha! What the hell! I will ride back home, Atlanta and smoke some weed baby, what the hell are gonna do with the damn money?” (Hahah! Nitaendesha gari langu kurudi nyumbani, Atlanta na kupiga madawa, utazifanyia nini fedha zako?) aliuliza jamaa mwingine baada ya kujitamba.

    “I ain’t do a lot of damn things, just spendin’ my time with some fucking bitches, smoke some weed,” (sitofanya mishe nyingi, nitatanua muda wote na malaya, kuvuta bangi kwa wingi) alisema jamaa huyo mwingine.

    Walikuwa wakizungumza kwa mbwembwe, mbele yao walijiona wakiwa na fedha nyingi kutokana kwa kile walichotakiwa kukifanya, walifurahia kwa kuwa hawakuona kama kungekuwa na mtu yeyote yule ambaye angewazuia.

    Wakati wakiendelea kula na kunywa huku tena wakivuta bangi, Vivian alikuwa chumbani kule alipojificha, alikuwa akimuomba Mungu amlinde kwani sehemu hiyo haikuwa salama hata mara moja.

    Aliyasikiliza mazungumzo yao lakini bado hakujua yule mtu aliyeletwa ndani ya chumba kile alikuwa nani. Alichokifanya, tena kwa mwendo wa kunyata akaanza kuondoka kuelekea katika chumba kile, kilikuwa na giza totoro kama kilivyokuwa kile chumba alichoingizwa yeye.

    Alipofika humo, akaanza kumuita David kwa kutumia jina la mwanaume huku akimwambia kabisa kwamba yeye hakuwa mtu mbaya, alikuwa mtu mzuri ambaye alifika hapo kwa ajili ya kumkomboa.

    “Who the hell are you?” (Wewe nani?) aliuliza David.

    “Vivian...”

    “Vivian...Benjamin’s girlfriend?” (Vivian...mpenzi wa Benjamin?) aliuliza David.

    “Yes!”

    “What the hell are you doing here?” (Unafanya nini hapa?)

    “I was kindnaped like you!” (nilitekwa kama wewe) alijibu Vivian.

    Wakati akizungumza hayo, tayari alikuwa amekwishamfikia Benjamin na hivyo kumfungua kamba alizokuwa amefungwa na kuanza kupanga mipango ya kutoka ndani ya nyumba hiyo.

    Alichokisema David kilikuwa ni kuondoka kupitia vyumba vingine kwani watu hao walikuwa sebuleni hivyo kama wangefanikiwa kufika katika vyumba vingine ingekuwa rahisi kwao kutoroka.

    “Haiwezekani!” alisema Vivian.

    “Kwa nini?”

    “Kila chumba kina dirisha la kioo kisichovunjika, nilijaribu kutoroka lakini nimeshindwa,” alisema Vivian.

    Ndiyo, kutoroka lilikuwa jambo lisilowezekana hata kidogo kwani Vivian alishajaribu kufanya hivyo lakini akashindwa. David hakutaka kukubali, kwake aliona kama msichana huyo alimdanganya hivyo kuanza kwenda katika vyumba hivyo kwa mwendo wa kunyata kwa kuamini kwamba wangeweza kufanikiwa.

    Matokeo yalikuwa yaleyale kwamba hawakuweza kutoka ndani hivyo kugundua kwamba sehemu ya kutorokea ilikuwa moja tu, nayo ilikuwa ni pale sebuleni.

    “Lazima tufanye kitu!” alisema David.

    “Kitu gani?”

    “Kupambana! Hakuna kingine zaidi ya hicho,” alisema David.

    “Tutapambana vipi?”

    “Subiri kwanza...”

    Akili ya David ilicheza harakaharaka, hakuona kama Vivian alikuwa na wazo lolote lile. Alikumbuka kwamba chumba alichokuwa amehifadhiwa kilikuwa na giza totoro hivyo ingekuwa rahisi kwake kufanya jambo na hatimaye kujinasua kutoka katika mikono ya watu hao. Akaanza kuvua nguo zake.

    “Unafanya nini?” aliuliza Vivian huku akionekana kushangaa.

    “Vua nguo zako pia!”

    “Ili?”

    “Nipe nivae na wewe uvae hizi,” alisema David.

    “Ili?”

    “Fanya hivyo Vivian, hatuna muda wa kupoteza,” alisema David.

    Kwa sababu yeye ndiye alikuwa amepata wazo juu ya nini cha kufanya, Vivian hakuwa na sababu ya kukataa, akavua nguo zake harakaharaka kisha kubadilishana na David na kuelekea ndani ya chumba kile huku David akichukua nondo kubwa iliyokaa kama fimbo na kuanza kurudi kule ndani.

    “Wewe utalala chini, kule pembeni, hakikisha ukilala, unafichan kichwa chako ukutani, halafu mimi nitasimama nyuma ya huu mlango, umesikia?” alisema David na kuuliza swali.

    “Ndiyo!”

    “Basi fanya hivyo,” alisema David.

    Vivian akaelekea pembeni kabisa, akalala kiubavuubavu, kichwa kilikuwa ukutani huku David akisimama nje ya mlango. Kila kitu kilipokuwa tayari, David akaanza kuupiga kelele akiwahitaji wanaume wale waje ndani ya chumba kile.

    “Bora nife, mbona mnaogopa kuniua? Mnaniweka humu ndani ili iweje? Kama wanaume kweli, mliozoea kuua, kwa nini msiniue,” alisema David kwa kupiga kelele, aliendelea kusema maneno hayo zaidi na zaidi kwa kuamini kwamba ni lazima vijana wale wangemfuata ndani ya chumba kile.





    Wanaume watatu wenye uchu wa fedha walikuwa wamekaa sebuleni, chupa kubwa za pombe zilikuwa mezani na walikuwa wakinywa mfululizo, maisha yao yalionekana kubadilika kwani kitu walichokuwa wakikitaka, walikipata na kazi moja tu ndiyo iliyokuwa ikisubiriwa, kumuua mtu ambaye waliambiwa wamuue.

    Mbele yao hakukuwa na kazi kubwa, kazi kubwa ambayo walikuwa nayo ni kumtafuta mtu huyo, baada ya kumpata, hakukuwa na kazi nyingine yoyote ile kwani kitendo cha kumuua, wala hakikuwa kazi kubwa, ilikuwa nyepesi sana, kama kumsukuma mlevi katika mteremko wa mlima Kitonga.

    Walipokuwa wakiendelea kunywa pombe kali, ndipo waliposikia kelele kutoka katika chumba walichomuhifadhi David, walikumbuka kwamba walimsiba mdomo kwa kutumia gundi hivyo wakajua kwamba kijana huyo alileta ubishi na hatimaye kutoa gundi hiyo mdomoni.

    Hilo liliwakasirisha sana, wawili wakamwambia mwenzao achukue bastola na kuelekea huko chumbani ili amtulize David, baada ya kunywa pombe ndipo wamuue kwa kumtumbukiza ndani ya pipa la tindikali.

    “Kamtulize, akileta ubishi, mzimishe kwa muda,” alisema Cobra.

    “Ila mnanionea sana, tunakunywa na kufurahia maisha, mnaanza kunituma,” alisema jamaa huyo aliyejulikana kwa jina la Amazon.

    “Wewe nenda, kwanza wewe si ndiye mdogo, hatumalizi pombe zote,” alisema Cobra huku akimwangalia Amazon kwa jicho lililomtaka kufanya kile alichomwambia.

    Huku akionekana kukasirika, Amazon akainuka, akachukua bunduki na tochi kisha kwenda katika chumba kile alichoambiwa aende. David hakunyamaza, aliendelea kuzungumza maneno yaleyale ya kuwatia hasira kwa kudai kwamba waliogopa kumuua.

    Alipoufikia mlango ule, akawasha tochi na kuingia ndani, alipomulika, mtu aliyemuona akiwa amelala, hakumuona vizuri, alimuona kwa nyuma tu, kutokana na mavazi aliyokuwa nayo, aliamini kwamba alikuwa David, akaanza kumfuata pale chini.

    Alipomfikia na kumwangalia vizuri, nywele nyingi alizokuwa nazo zilimshtua, alipotaka kugeuka tu, akashtukia akipigwa nondo ya kichwa, hapohapo akaanguka chini na kupoteza fahamu.

    “Inuka...inuka Vivian,” alisema David huku akimuinua Vivian.

    Vivian akainuka, David akachukua bastola ile na kumwambia Vivian amfuate, wakaanza kuelekea sebuleni. Walipofika huko, wakamkuta Cobra na mwenzake wakinywa pombe kali, hapohapo wakawaweka chini ya ulinzi.

    “Ukitingishika tu, nakumwaga ubongo,” alisema David huku akionekana kuwa na hasira.

    Wote wakatulia, kwa jinsi David alivyoonekana, alionekana kuwa na hasira nyingi ambaye hakutaka kabisa kufanyiwa mchezo. Walibaki wakiwa wametulia na kufanya kile ambacho David alitaka wakifanye.

    Alichowaambia ni kwamba wachukue simu na kumpigia mtu ambaye aliwatuma na kumwambia kwamba kazi ilikuwa imekamilika, yaani yeye na Vivian walikuwa wamekufa.

    Hakukuwa na aliyeleta ubishi kwani walijua kwamba kijana huyo hakuwa na masihara hata kidogo hivyo wakachukua simu na kumpigia Dracula. Simu iliita kwa muda mchache tu, ikapokelewa.

    “Mmekamilisha?” ilisikika sauti ya Dracula kutoka upande wa pili.

    “Kila kitu tayari! Tumewaua wote,” alisema Cobra.

    “Safi sana! Ngoja niwasiliane na mzee, kiasi kilichobaki kitatumwa katika akaunti zenu,” alisema Dracula kisha Cobra kukata simu.

    Hiyo wala haikutosha, alichoagiza David ni kwamba Vivian awafunge kamba na kisha waondoke, hilo wala halikuwa tatizo, Vivvian akarudi chumbani kule ambapo alimkuta Amazon akiwa hoi chini huku damu zikimtoka kichwani, akachukua kamba na kurudi sebuleni ambapo akawafunga vijana hao na wao kuondoka huku wakiufunga mlango kwa nje.

    ****

    Dracula alikuwa akizungumza na Bwana Seppy katika kituo cha polisi, muda wote uso wa mzee huyo ulionyesha tabasamu pana kwani hakuamini kile alichokisikia kwamba mtu aliyekuwa akimsumbua kwa wakati huo alikuwa marehemu.

    Hiyo ilimaanisha kwamba hakukuwa na mtu yeyote ambaye angemtisha katika kesi hiyo kwani kama shahidi aliyekuwa akimtegemea Benjamin alikuwa mmoja tu, David ambaye mpaka katika kipindi hicho alipewa taarifa kwamba alikuwa marehemu.

    “Una uhakika wamefanikiwa?” aliuliza Bwana Seppy.

    “Ndiyo! Wamenipa taarifa, huwa wanafanya hivi kila siku,” alisema Dracula.

    “Asante Mungu!”

    Hakuwa na cha kufanya zaidi ya kumshukuru Mungu tu, kwake ulionekana kuwa kama muujiza mkubwa kwani kwa kipindi hicho alihitaji sana David auawe kuliko kitu chochote kile.

    Alibaki akiiangalia saa yake, aliona muda ukikawia kwenda kwani alitamani kusimama kizimbani na kuiambia mahakama kwamba hakuwa amefanya mauaji na kama wanabisha walete shahidi kitu ambacho ingekuwa ngumu kwa Benjamin na watu wake kufanya hivyo.

    Upande wa pili ulikuwa ni kilio tu, taarifa zilianza kusambaa kwamba David alikuwa ameuawa, hakukuwa na siri tena, kwa Benjamin, tayari alikata tamaa, muda wote alionekana kuwa na huzuni tele kwani kwa namna moja au nyingine lazima mahakama ingemhukumu kifo au hata kufungwa kifungo cha maisha gerezani.

    Alizungumza na mwanasheria wake, Donald na kumwambia wazi kwamba alikuwa na hofu moyoni mwake, kama ilivyokuwa kwa Benjamin, hata kwa Donald ilikuwa hivyohivyo kwani aliamini kwamba David aliuawa lakini napo ilikuwa ngumu kusema kwamba Bwana Seppy ndiye alikuwa amehusika kwani wangeulizwa kama wana ushahidi kitu ambacho kingewapa wakati mgumu.

    “Kwa hiyo tufanye nini?” aliulizaDonald.

    “Duh! Yaani siwezi kuamini kama David ameuawa, na FBI wanasemaje?” aliuliza Benjamin huku akionekana kuchanganyikiwa.

    “Wamejaribu kumtafuta...”

    “Ikawaje?”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Nao wakamkosa.”

    “Hata mwili wake?”

    “Nao wameukosa pia,” alijibu Donald.

    Benjamin akaona huo ndiyo mwisho wake, alipoambiwa hivyo na Donald, hakutaka kuendelea kuzungumza naye, akaomba kuondoka kwani kichwa chake kilichanganyikiwa mno.

    Siku hiyo haikuwa nzuri katika maisha yake, alipagawa kwa sababu mtu pekee ambaye alibaki, aliyekuwa tegemeo lake alikuwa David tu ambaye mpaka muda huo tetesi zilisema kwamba aliuawa kwani hakuwepo nyumbani na wala hakuonekana sehemu yoyote ile.

    “Mungu nisaidie!” alisema Benjamin huku akiwa amepiga magoti, alionekana kukata tamaa kwa asilimia mia moja.

    ****

    Siku hazikumsubiri mtu, ziliendelea kukatika, Moyo wa Benjamin ulikuwa kwenye maumivu makali mno hasa baada ya kugundua kwamba mshikaji wake aliyekuwa na ushahirdi wote, David alikuwa amepotea katika mazingira ya kutatanisha.

    Hakukaa kimya, aliwaambia wazazi wake juu ya hofu aliyokuwa nayo moyoni mwake, aliwaambia wazi kwamba kila siku alikuwa mtu wa mawazo na hakujua kama ingetokea siku yoyote ile angeweza kupata furaha aliyokuwa nayo kabla kama tu huyo David asingepatikana.

    “I don’t know what I should do but the world must know that I killed nobody,” (Sijui ninachotakiwa kufanya lakini lazima dunia ijue sijamuua mtu yeyote yule) alisema Benjamin huku akiwa ameuinamisha uso wake.

    “Everybody knows you killed nobody, but we have to look for the evidence to set you free,” (Kila mtu anajua hujamuua mtu yeyote yule lakini ni lazima tuutafute ushahidi) alisema baba yake.

    “Nobody knows where David is by now, they killed him, why? When I come back, I’ve to tell the world about what happened although David disappeared” (Hakuna anayejua mahali David alipo kwa sasa, watakuwa wamemuua, kwa nini? Nitakaporudi, nitatakiwa kuiambia dunia kila kitu kilichotokea hata kama David amepotea) alisema Benjamin huku machozi yakianza kumtoka.

    Hakukuwa na kilichobadilika, bado Benjamin alitakiwa kukaa jela mpaka pale ambapo angeitwa tena mahakamani. Ushahidi mwingine ukakusanywa na hivyo kilichokuwa kikitakiwa ni siku ya mahakama ifike na kila kitu kuwekwa wazi.

    Siku ilipofika, tayari watu wengi walikwishakusanyika ndani ya mahakama hiyo. Hali ilikuwa tofauti na kipindi cha nyuma. Watu walibadilika, hawakutaka tena kuona Benjamin akifungwa bali Bwana Seppy ndiye alitakiwa kufungwa kutokana na kile alichokifanya.

    Waandishi wa habari walikuwa ndani ya mahakama hiyo, walitaka kuandika kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Mwana huo wa 2011, hakukuwa na kesi iliyovuta hisia za watu wengi kama hiyo.

    Kila mtu duniani alitegesha masikio yake kusikiliza kile kilichokuwa kikiendelea katika mahakama hiyo huko nchini Marekani. Jaji yuleyule, McRegan ndiye aliyetakiwa kusikiliza kesi hiyo na kutoa hukumu.

    Mahakama ilijaza watu, hakukuwa na nafasi ya watu wengine na hata wale waliokuwa wamechelewa ambao walikuwa ni zaidi ya watu elfu kumi walitakiwa kubaki nje na kufuatilia kesi ile kupitia televisheni kubwa iliyowekwa tayari nje ya mahakama hiyo.

    Haukupita muda mrefu, basi kubwa lililobeba watuhumiwa likaanza kuingia ndani ya eneo la mahakama hiyo. Waandishi wa habari ambao walikuwa nje wakalisogelea gari hilo na kuanza kulipiga picha.

    Basi liliposimama, mahabusu kadhaa wakaanza kuteremka huku wakiwa na pingu mikononi mwao. Miongoni mwa mahabusu hao alikuwa Benjamin na Bwana Seppy ambaye muda wote uso wake ulikuwa na tabasamu pana.

    Alichokuwa akifahamu, David alikuwa ameuawa kama alivyoambiwa na Dracula, alijua kwamba Benjamin hakuwa na ushahidi wowote ule ambao ungemuweka matatani.

    Aliwapungia watu mikono, watu wengi walikuwa wakimzomea lakini hakuonekana kujali mpaka alipoingia ndani ya mahakama. Watu walitaka kuisikiliza kesi hiyo na hukumu kutolewa siku hiyohiyo, hakukuwa na mtu aliyefika mahali hapo kwa ajili ya kusikiliza kesi nyingine yoyote ile.

    Wakati Jaji McRegan anaingia ndani ya mahakama hiyo, watu wote wakasimama kama ishara ya heshima, jaji akatembea mpaka mbele ambapo akakaa katika kiti chake kisha kuwaruhusu watu kukaa kwa kupiga nyundo yake.

    Muda wote Benjamin alikuwa amekiinamisha kichwa chake chini, alionekana kuwa na majonzi mazito na muda wote machozi yalikuwa yakimtoka tu. Wakili wake, Donald ndiye aliyekuwa akimsimamia siku hiyo, mbali na huyo, pia kulikuwa na wakili wa upande wa Bwana Seppy, wakili huyu aliitwa Tedd, mwanaume mrefu ambaye muda wote alivalia miwani.

    Zilianza kusikiliza kesi nyingine ambazo zilichukua masaa mawili na ndipo Benjamin akatakiwa kupanda kizimbani. Watu walikuwa wakimwangalia tu, alionekana kuwa na maumivu makali moyoni mwake kiasi kwamba hata watu wengine wote wakaanza kumuonea huruma.

    “Unaitwa nani?” aliuliza Donald.

    “Naitwa Benjamin Saunders.”

    “Unajua kwa nini upo hapa?”

    “Ndiyo! Ni kwa sababu mahakama inanihusisha na mauaji yaliyotokea,” alijibu Benjamin.

    “Mnamo tarehe ishirini mwezi wa sita mwaka jana, kulikuwa na mauaji yaliyotokea, mwanamuziki, Carter Phillip alikutwa amekufa katika chumba kimoja huko Southampton nchini Uingereza, polisi walifanya kazi yao na kugundua kwamba alama zako za vidole zilikutwa katika mwili wa marehemu, na si kwenye mwili tu bali hata katika sehemu nyingine chumbani humo, unalizungumziaje hilo?” alisema Donald na kuuliza swali.

    “Kitu cha kwanza ambacho mahakama hii inatakiwa kufahamu ni kwamba sikuwahi kuua katika maisha yangu. Nilimfahamu Carter kama mwanamuziki chipukizi. Mnamo tarehe tano mwezi wa saba nilipokea simu ya kuhitajika sehemu fulani, huko nilipokwenda, nilikutana na Bwana Seppy ambaye alinipa kazi ya kufanya mauaji ya Carter Phillip. Sikujua sababu ila nilimkatalia kwa kuwa sikuwahi kuua,” alisema Benjamin.

    “Unahisi kwa nini alikuchukua wewe?”

    “Mimi ni mtaalamu wa kompyuta, aliamini kwamba kama ningeifanya kazi yake ingekuwa nyepesi na hata kugundulika ingekuwa ngumu. Kwa kweli nilikataa kabisa,” alisema.

    Huo ulikuwa ni muda wa maswali kutoka kwa wakili wake, maswali yake yalikuwa ya kumpa nafasi ya kuelekezea kile kilichokuwa kimetokea, wakili Donald alichukua dakika kumi, alipomaliza maswali yake, akakaa chini na wakili wa Bwana Seppy kusimama.



    Maswali yake yalikuwa magumu lakini Benjamin alijitahidi kujibu kwa uelewa mkubwa, baada ya kuulizwa maswali hayo na kumaliza, hapo ndipo akakaa, watu wote wakata kuona Bwana Seppy naye akiulizwa maswali.

    Hilo halikuwa tatizo, akasimama na kuelekea kizimbani. Mtu wa kwanza kabisa kumuuliza maswali alikuwa wakili wake, maswali aliyoulizwa yalikuwa mepesi na yale ya kumuweka katika wakati mzuri wa kushinda kesi, wakili huyo alipomaliza, akasimama na Donald kusimama.

    “Unaitwa nani?” aliuliza Donald huku akimwangalia Bwana Seppy usoni mwake.

    “Naitwa David Seppy...”

    “Sawa. Una akili?” aliuliza Donald.

    “Unasemaje?”

    “Una akili?” alirudia swali lake.

    “Ndiyo nina akili!”

    “Unajua kwa nini upo hapa?”

    “Ndiyo mheshimiwa! Nipo hapa kwa sababu nimesingiziwa kwamba nimeua,” alisema Bwana Seppy.

    “Umesingiziwa au umeua kweli?”

    “Nimesingiziwa kwa kuwa kama ningekuwa nimeua, basi hata alama za vidole vyangu zingeonekana,” alijitetea.

    “Mshtakiwa ambaye ni Benjamin anasema kwamba wewe ndiye uliyehusika katika mauaji hayo na wewe ndiye uliyemuita na kumpa kazi hiyo ili akaue, ni kweli?” aliuliza Donald.

    “Si kweli!”

    “Unamjua Benjamin? Ushawahi kuonana naye kabla?” aliuliza Donald.

    “Hapana! Sikuwahi kuonana naye kabla.”

    “Una uhakika?”

    “Ndiyo mheshimiwa.”

    “Tarehe kumi na mbili mwezi wa sita, simu yako ilitumika kutuma ujumbe mfupi kwenda namba +56 890 672 88 ambayo inamilikiwa na mtu anayejulikana kwa jina la Petterson Edward ambaye ulikuwa ukimuita kwa jina la Dracula, ujumbe huo uliuandika kwamba kulikuwa na mtu ambaye alitakiwa kuuawa mara moja, huyo si mwingine bali ni Carter, ni kweli?” aliuliza Donald.

    “Si kweli!” alijibu Bwana Seppy baada ya kukaa kimya kwa muda.

    “Mheshimiwa hakimu, naomba niwekewe televisheni na kompyuta kwa ajili ya kuletea ushahidi ulioshiba kabla ya shahidi wa mwisho kabisa ambaye ni David kuja na kuthibitisha yote yaliyotokea,” alisema Donald.

    Bwana Seppy alipolisikia jina la David, akayapeleka macho yake kwa Dracula ambaye alikuwa ndani mahakama ile, alichanganyikiwa kwani taarifa ya mwisho ilisema kwamba mtu huyo alikuwa ameuawa, je, ni David yupi ambaye alikuwa akizungumziwa mahali hapo.

    Hakukuwa na muda wa kupoteza, harakaharaka televisheni ikaletwa mahali hapo, laptop ikaunganishwa na simu simu aina ya iPhone aliyokuwa nayo Donald na kisha kuanza kuonyesha ushahidi wa kila kitu kilichokuwa kimetokea.

    “Kama nilivyosema, ushahidi umeonyesha kufanya mawasiliano hayo kama inavyoonekana, ujumbe huo ulitumwa kutoka namba hii, naomba kuuliza, je, hii namba ni yako au si yako?” aliuliza Donald huku akimuonyeshea namba Bwana Seppy katika televisheni.

    “Ni yangu!”

    “Kuna mtu aliwahi kuishika simu yako na kutuma ujumbe pasipo kujua?” aliuliza.

    “Hapana!”

    “Sawa. Mnamo tarehe kumi na tisa mwezi wa tisa, ujumbe wa mauaji ulitumwa kutoka katika simu yako kwenda katika namba ileile na ulisema kwamba ni lazima Todd Lewis auawe kwa sababu alikataa kuweka mkataba na wewe ambao ungemlipa kiasi kidogo cha fedha, hivyo kama kisasi ukaamua kumuua kwa kutuma watu, je, ni kweli?” aliuliza Donald, Bwana Seppy akabaki kimya, alianza kuweweseka huku akiangalia huku na kule.

    “Uliidanganya dunia kwamba Benjamin ndiye aliyekuwa akifanya mauaji. Hiyo haikutosha, pia ulitumia njia hizohizo kuwaua watu wengine na kumfanya Benjamin kuingia matatani. Na kwa faida ya mahakama ni kwamba ulikuwa ukiweka noti kila sehemu uliyoua ili iwe vigumu kugundulika ila noti hizo zilikuwa na maana kubwa.

    “Ile noti ya Dola, alama yake ambayo inawakilisha S, ile Euro ambayo inawakilisha fedha ya Ulaya, ile Paundi iliyowakilishwa na P, na mwisho ile Yuen iliyowakilishwa na Y, inaunganisha jina lako la SEPPY, je, bado unataka kubisha hapo?” aliuliza Donald huku akimwangalia mzee huyo usoni. Bwana Seppy akabaki kimya.

    “Wiki kadhaa zilizopita, kulikuwa na mauaji ya msichana Stacie, mauaji hayo yalifanyika jijini Los Angeles mnamo majira ya saa nne usiku huku alama za vidole zikionyesha kwamba ni Benjamin ndiye aliyehusika, saa tano usiku kupitia kamera za CCTV zilizokuwa Boston zilimuona Benjamin na hivyo polisi kwenda kumkamata.

    “Swali langu ni hili! Kama ni Benjamin ndiye aliyekuwa amefanya mauaji ya Stacie, je, alitumia usafiri gani kutoka Los Angeles mpaka Boston na wakati kutoka sehemu hizo kwenda nyingine hutumia muda wa saa tatu kwa usafiri wa treni na saa mbili na nusu kwa usafiri wa ndege? Wewe ndiye uliyefanya mauaji hayo, na bahati mbaya sana ulishindwa kujipanga kwa kutumia saa yako,” alisema Donald huku akiifunga faili lake.

    Bwana Seppy alibaki kimya, alikuwa akitetemeka mno, hakuamini kile kilichokuwa kikiendelea mahakamani hapo, alimwangalia Donald huku akionekana kuchanganyikiwa.

    Minong’ono ilianza kusikika hapo mahakamani, kesi ilionekana kuwa nyepesi mno kwa upande wa Benjamin. Wakati Donald akilifunga faili lake, hapohapo akamuomba mheshimiwa jaji kumruhusu kumleta shahidi wa mwisho, huyo shahidi wa mwisho akaruhusiwa kuingia hapo mahakamani, kitu kilichomshtua Bwana Seppy, ni David na msichana Vivian wakaingia.

    “Aliuawa, nini kinaendelea?” alijiuliza Bwana Seppy, hapohapo akaona huo ndiyo mwisho wake.

    “Mheshimiwa jaji, naomba tumpe nafasi shahidi, hii ni kesi nzito ambayo inahitaji ushahidi wa kutosha kwani kama shahidi hatotoa ushahidi wake hapa mahakamani sasa hivi, anaweza kuuawa kwani hata alipotajwa kwamba yeye ni shahidi, alitekwa,” alisema Donald na kumuomba hakimu, hapohapo David akapanda kizimbani na kuanza kutoa ushahidi wake.

    “Mheshimiwa jaji, mara baada ya rafiki yangu Benjamin kupata tatizo, aliniomba nimsaidie ili kujua kilichokuwa kikiendelea nyuma ya pazia, ilikuwa kazi kubwa na nzito lakini kwa kutumia kompyuta yangu, niliweza kufanikiwa kunasa ushahidi wote ambao niliukabidhi kwa Donald.

    “Kwa kifupi ni kwamba Bwana Seppy amehusika katika mauaji. Baada ya kujua kwamba mimi ndiye shahidi kwa kuwa data zote ninazo, akawatuma watu waje kuniteka, wakaniteka na kunipeleka katika jumba moja lipo sehemu fulani.

    “Huko nikakutana na huyu msichana, Vivian ambaye ni mpenzi wa Benjamin, alinihadithia kilichotokea baada ya kutoroka. Tulipotoroka, kitu cha kwanza kilikuwa ni kumtafuta Donald ambaye akatupeleka katika jengo la FBI ambapo tulipewa hifadhi kwani bila kufanya hivyo, tungeuawa.

    “Ila mbali na kufanya mauaji ya watu hao, nadhani pia anatakiwa kushtakiwa kwa kufanya mauaji ya maofisa wa FBI kwani wakati amewatuma vijana wake kumteka Benjamin, waliua maofisa wa FBI na kumteka Vivian,” alisema David.

    David alizungumza mambo mengi yaliyokuwa yametokea, kila alipokuwa akizungumza, watu walikuwa kimya wakimwangalia tu, jaji McRegan alikuwa akiandika kila kitu kilichokuwa kikihitajika kuandikwa. Mpaka David ananyamaza, alikuwa ameridhika na ushahidi.

    Jaji akabaki kimya, watu wote walikuwa wakimsikilizia yeye ni kitu gani angezungumza baada ya kupewa ushahidi uliojitosheleza. Hakutaka kutoa hukumu moja kwa moja, alichokifanya ni kuliita jopo la wazee wa baraza, wakaomba muda wa dakika ishirini kwa ajili ya kuijadili kesi hiyo.

    Minong’ono haikuisha hapo mahakamani, kila mtu alikuwa akiongea lake huku wakimtaka jaji amuhukumu Bwana Seppy kifungo cha maisha gerezani au hata kumnyonga kutokana na kile alichokifanya.

    Jopo hilo la wazee wa baraza na jaji lilichukua dakika kumi na tisa, likarudi mahakamani. Kabla ya kuzungumza kitu chochote kile, jaji akaanza kuwaangalia watu waliokusanyika ndani ya mahakama hiyo kisha kuyapeleka macho yake kwa Bwana Seppy.

    Mwanaume aliyekuwa bilionea, aliyewatetemesha watu wengi kwa ajili ya ubilionea wake, leo hii alikuwa kizimbani huku akituhumiwa kuua watu kwa tamaa zake za fedha.

    Mbali na yeye, pia kulikuwa na familia yake, muda wote mke wake alikuwa akilia, hakuwa akiamini kile kilichokuwa kikiendelea mahakamani hapo. Watoto wake waliokuwa na miaka kumi na tisa nao walikuwa pamoja nao, kitendo cha baba yao kufikishwa mahakamani tu kisa aliua kiwahuzunisha wote na hawakutegemea kama kitu kama kile kingetokea.

    “Mahakama imejiridhisha kwa kila kitu kilichotokea, ushahidi umekamilika na kila kitu kilichozungumzwa. Hivyo kwa kupitia kifungu namba 113B kilichowekwa mwaka 1893, mahakama haikumkuta Benjamin na hatia hivyo inamuachia huru ila kwa mauaji aliyoyafanya David Seppy, amekutwa na hatia hivyo atahukumiwa kifo kwa kuchomwa sindano ya cyanide mpaka kifo.

    “Hii itakuwa fundisho na pia kwa kupitia maofisa wa FBI, imebainika kwamba mmoja wa watu wake ambao walikuwa wakifanya mauaji ajulikanaye kwa jina la Petterson Edward ‘Dracula’ yupo hapa mahakamani akifuatilia kila kitu, hivyo naye atachukuliwa na kujumuishwa katika adhabu hii,” alisema jaji, hakutaka kuendelea sana, akapiga nyundo yake, akasimama na kutoka katika kiti kile.

    Mahakama nzima ilikuwa shangwe, watu hawakuamini kama kweli kile walichokisikia ndicho kilichokuwa uamuzi wa mahakama ile. Benjamin hakutaka kusubiri, hapohapo akachomoka na kuwafuata wazazi wake na kuwakumbatia, kwake, ilikuwa furaha tele.

    Kwa Bwana Seppy ilikuwa ni kilio kikubwa, hakuamini kile ambacho mahakama ilikiamua, akabaki akilia pale alipokuwa. Hata kabla watu hawajawanyika, tayari maofisa wa FBI walimfikia Dracula na hapohapo kumpiga pingu na kuondoka naye.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Siku iliyofuata, magazeti yote nchini Marekani yalitawaliwa na habari hiyo, kifo cha Bwana Seppy ambaye katika kipindi hicho ndiyo alitakiwa kuanza maandalizi ya kuiaga familia yake kabla ya kutekelezwa adhabu kali ya kifo ambayo ilikuwa mbele yake.

    Alilia na kuhuzunika sana lakini hakuweza kubadilisha kitu chochote kile, hukumu ilikuwa palepale kwamba ni lazima afe kama hukumu ilivyosomwa mahakamani.

    Benjamin akabadilika na kuwa shujaa, yule mtu aliyekuwa akitafutwa usiku na mchana, akawa mtu aliyekuwa akipendwa na kuzungumziwa kila kona, kila mtu alitamani kuwa karibu naye japo kupiga picha naye kwani hakukuwa na mtu aliyeonekana kuwa shujaa kama alivyokuwa yeye.

    Alichokifanya ni kuendelea na masomo yake chuoni na baada ya miaka miwili, akakamilisha miaka yake mitano ya kusomea masuala ya kitabibu na hivyo kuwa daktari katika Hospitali ya St. Monica iliyokuwa Ohio nchini Marekani.

    Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa mafanikio yake, hakumuacha mpenzi wake, Vivian, baada ya miaka miwili kukatika, akamuoa kwa harusi kubwa na iliyohudhuriwa na watu wengi maarufu.

    Kilichoendelea baada ya hapo, kilikuwa ni historia tu.



    MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Blog