Search This Blog

Friday 18 November 2022

MPANGO WA SIRI - 3

 






Simulizi : Mpango Wa Siri
Sehemu Ya Tatu (3)




Lee alikuwa fundi wa kupigana. Tangu mdogo alipokuwa anasoma shule ya Msingi Masoko, Lee alisifika kwa sifa kuu tatu. Ukorofi,ubishi na tamaa. Lee alikuwa mkorofi sana. Nusu ya wanafunzi wa kiume wa shule ile alikuwa kashapigana nao. Hata baadhi ya wanafunzi wa shule za jirani za Mnazimmoja na Mtanga alikuwa kashaoneshana nao ubabe.

Lee alikuwa mbishi. Mbishi kwa walimu wake, mbishi kwa wazazi wake, mbishi kwa wanafunzi wenzake na jamii nzima iliyomzunguka. Lee alikuwa humtumi bure, mpaka umpe hela ndipo atumike.Hapo ndipo sifa yake ya tatu ilipojidhihirisha. Sifa ya tamaa, tamaa ya pesa.



Lee alikuwa mcheza kamari maarufu tangu akiwa mtoto. Alipofika darasa la tano aligundua aina mpya ya kamari. Kamari ya kupigana mshindi anapewa pesa. Lee ndiye alikuwa mwanzilishi wa kamari hiyo.Karibu na shule ya Msingi Masoko Kulikuwa na bonde maarufu kama Bokorani, huko ndiko kulikuwa uwanja wa mapambano. Lee ndiye alikuwa bingwa wao.



Alimaliza darasa la saba kwa shida na mikutuo mingi sana. Hakutaka kuendelea na elimu ya Sekondari. Lee alijiunga na magenge ya kihuni. Ambayo kazi yao kubwa Ilikuwa ni wizi wa majumbani baada ya kuvuta bangi na kutumia madawa ya kulevya.

Huko ndipo alipokulia na ndiko alipokutana na Chao. Kijana mtukutu aliyeshindikana duniani. Mwanachama wa Ocafona.Na ambaye ndie alimuingiza Lee katika kundi hili la kihalifu la Ocafona .



Baada ya matukio mengi ya mauaji waliyoyafanya ndani ya kundi hili sehemu mbali mbali nchini. Ndipo Lee alipewa cheo cha kusimamia mpango huu haramu. Aliitwa jina la Lee kutokana na kukubuhu kwake kimapigano Kwa kutumia mitindo yote ya Kichina, tena bila kufundishwa na mtu yoyote. Kwa majina yake kamili alikuwa anaitwa Zedi Nungwi...



****http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Lee alikuwa anamsogelea Mirambo akipiga makofi na kutabasamu. Mzee Mirambo alisimama imara akiwa hana wasiwasi hata chembe.



Mpambano wa pili ulianza.



Lee alirusha ngumi kali iliyokuwa inaelekea chini ya kidevu cha Mirambo, Mzee Mirambo aliiona vizuri ngumi ile, alirudi nyuma hatua moja ngumi ikapita, Lee alirusha teke kwa mguu wake wa kulia lililozuiliwa na Mzee Mirambo kwa mkono mmoja. Mguu uliokuja na teke lile haukurudi. Ulinaswa na mkono imara wa Mzee Mirambo. Mirambo akaupiga mtama ule mguu wa Lee uliobaki chini, aliupata, na huu mguu alioushika nao aliuachia. Lee alienda chini mzimamzima. Kwa haraka pale chini Lee aliinuka.

Aliinuka na nguvu mpya sasa. Alirusha teke lililoshiba lilitua sawia shingoni kwa mzee Mirambo. Mzee Mirambo alipepesuka kidogo. Akiwa bado katika mpepesuko alirusha ngumi iliyompata Lee tumboni. Lee aligumia kwa maumivu. Alishika tumbo lake, lilikuwa kosa la mwaka, ngumi tatu za nguvu zilitua usoni kwake..



Balaa...



Sasa Lee alipata mtihani, ashike tumbo au uso. Kabla hajapata jibu alipigwa ngwara iliyomzoa tena mzimamzima mpaka chini. Mzee Mirambo aligeuka mbogo sasa. Uwanja mzima uliguna kwa fadhaha.



Kule konani alipokaa Edgar aliona Bosi wao anaumbuka sasa. Alijipapasa kiunoni na kutoa bastola yake. Alimsogelea Mzee Mirambo huku akimuonesha ile bastola. Mzee Mirambo alinywea kidogo na kunyoosha mikono yake juu huku akitafuta mbinu ya kujitoa katika kisanga kile.

Edgar akamuita Edina na kumuamrisha amfunge pingu Mzee Mirambo. Mzee Mirambo alifungwa pingu chini ya ulinzi mkali. Watu wawili walimbeba bosi Lee na kumuingiza ndani. Mzee Mirambo nae walimpeleka kumfungia katika chumba cha mateso. Akisubiri kibano na kuuwawa bila shaka, Hakuna aliyewahi toka hai katika chumba kile cha kutisha!http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Kule ndani Lee akiwa anagugumia kwa maumivu aliisogelea kompyuta yake taratibu. Akafungua faili lililopewa jina la



" Watu wa kukaa nao mbali katika Mpango huu”



Yalikuwa majina ya watu watatu, picha na wasifu wao. Alipoangalia picha ya mtu wa tatu katika orodha ile alikutana na sura ya Mzee aliyetoka kupambana nae muda mfupi uliopita.



Lee aliiona hatari ya kukaa ma mzee yule nyumba moja. Aliamua kwenda kumuua kabla ya mambo hayajaharibika.

Lee akiwa na hasira ya kupigwa alinyanyuka. Alichukua bastola yake na kuelekea katika chumba cha mateso. Kwenda kummaliza Mzee Mirambo. Alipokaribia karibu na chumba cha mateso alistuka sana. Mlangoni alikutana na mwili wa mlinzi wa chumba cha mateso umelala tuli sakafuni. Ukiwa hauna roho!

Mlango ukiwa wazi unamchekea. Kuangalia ndani ya chumba kile cha mateso hakukuwa na mtu....Mzee Mirambo alikuwa ametoroka.



E bwana wee!!!



Mlango ukiwa wazi unamchekea. Kuangalia ndani ya chumba kile cha mateso hakukuwa na mtu...

Mzee Mirambo alikuwa ametoroka !



Walimtafuta ndani ya nyumba ile hawakumuona. Waliambulia miili kumi ya wafanyakazi wa Ocafona army ikiwa haina pumzi..

Cha kushangaza na kustaajabisha runinga yake Lee aliyoitegemea sana haikuonesha matukio ya mauaji yale. Lee alikiri kuwa Mzee Mirambo alikuwa jasusi wa kimataifa..



Baada ya kuambulia patupu ndani ya nyumba ile. Sasa walianza kutafuta Kisiwa kizima. Walikigeuza kisiwa nje ndani hawakufanikiwa kumuona Mzee Mirambo.

Ulianza msako mkali. Walitumia picha kuwaonesha watu wa Kisiwa kile kama wamemuona Mzee Mirambo. Bahati nzuri walikuwa na kumbukumbu ya picha za Mzee Mirambo katika kompyuta ya Bosi Lee, walizichapisha nyingi sana ili ziwasaidie katika msako.



Mtu anakunyima hela hakunyimi neno. Wahenga walisema. Walikutana Na Mvuvi mmoja aliwamwagia kila kitu.



"Namjua huyu Mzee anakuja sana, na mtoto wake anasoma shule ya Msingi Kisiwani "Mvuvi aliropoka mbele ya bosi Lee.

Walimshukuru kwa kumpa shilingi elfu kumi. Mvuvi yule aliondoka na kicheko hadi jino la mwisho lilionekana. Bila kujua huku nyuma ameacha dhahma kubwa.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Ocafona wakapanga mpango ukapangika. Walifanikiwa kumteka mtoto wa pekee wa Mzee Mirambo. Walilaza wanafunzi wote kwa kupulizia dawa na kufanikiwa kumchukua mtoto wa Mzee Mirambo, Nasri. Waliacha maiti moja tu nyuma. Maiti ya mlinzi wa shule ile aliyeonekana mbishi.

Kwa kumtumia Edina mtoto Nasri alimueleza kila kitu. Kikubwa walichokuwa wanakitaka ni kukujua nyumbani kwa Mzee Mirambo. Kwa kutumia mwanamke ilikuwa rahisi kumnyenga Nasri na kuwapeleka akina Kishoka nyumbani kwao.

Hadi wanafika nyumbani kwa Mzee Mirambo ilikuwa mnamo saa nane usiku. Ili kuogopa wasistukiwe walienda watu wanne tu. Edina, Edgar, Kishoka wakiwa wameambatana na mtoto Nasri. Huku wakituma taarifa kila dakika kwa bosi kila kinachoendelea.



Mke wa mzee Mirambo alikuwa amelala. Huku Mzee Mirambo akitafakari yaliyotokea jana yake. Alikumbuka jinsi alivyowekwa Katika chumba cha mateso akisubiri kusulibiwa na Lee na jinsi alivyofanikiwa kutoka hai.



Kilikuwa chumba kidogo kisichokuwa na dirisha hata moja. Hivyo kilikuwa na giza si mchana si usiku. Kilikuwa chumba chenye harufu, harufu nzito ya damu za watu. Kulikuwa na kiti kimoja cha mbao ambacho ndicho aliwekwa yeye.

Alikumbuka alivyosimama huku akiwa amefungwa pingu kwa nyuma. Aliipitisha mikono juu ya kichwa na mikono na ile pingu iligeukia mbele. Alikohoa kidogo.

Kiherehere cha mlinzi ndio kilichomponza. Aliposikia kikohozi alifungua mlango eti kuja kumwangalia mateka wake. Lilikuwa kosa la kiufundi. Mzee Mirambo alikuwa amebana nyuma ya mlango. Alipofungua tu mlango alikutana na robo yenye uzito wa kilo saba. Ilikuwa ni kukurukukuru ndani ya chumba. Kwa bahati nzuri mtazamaji wa runinga alienda chooni muda huo. Wakati Bosi anastarehe chooni mlinzi alikuwa akitaabika chumbani. Ile pingu ilisaidia kumbana mlinzi shingoni.

Alifanikiwa kumuua yule mlinzi huku akiwa ameshikilia bunduki yake aina ya SMG. Ndani ya mifuko ya mlinzi alifanikiwa kupata funguo za pingu. Baada ya kufungua pingu hapo ndipo mzee Mirambo alipokuwa makini na kamera za nyumba ile. Aliharibu kamera kabla haijamuona. Hadi anatoka nje ya jengo lile kamera tano na walinzi kumi walikuwa wameelekea kuzimu!



Alipofika ufukweni hakutaka kukodi boti. Alijua mwenye boti anaweza kutoa siri atakapokutana na Wanaharamu wale. Mzee Mirambo alikuwa na balaa. Alipiga maji, aliogelea toka Kilwa Kisiwani hadi Kilwa Masoko.Wakati anawaza hayo yaliyotokea mchana ghafla alianza kusinzia. Usingizi ulimjia ghafla. Alianza kushindana na macho yake. Hakutaka kulala, alikuwa anataka kufikiria cha kufanya ilI kutatua kadhia hili. Hakuweza kushindana na dawa za kina Edgar. Alilala, na ndio ulikuwa usingizi wake wa mwisho.



****



Wakati uliopo..



Daniel Mwaseba alikuwa anaingia Kilwa Masoko sasa. Kuja kutatua mchezo huu. Gari alilitelekeza kijiji cha Mpara. Pori kwa pori aliingia mjini Masoko. Alifikia nyumba ya wageni ya Bwawani. Alipaona ndipo mahali salama pa kuanzia msako wake. Akiwa katika chumba namba 6 katika hoteli ya Bwawani, Daniel alikuwa anawaza juu ya kisanga hiki. Kwa kuwa aliitaka mwenyewe kazi ya kuwafichua waovu hawa sasa aliingia kamili kazini.

Alikumbuka mauaji waliyoyafanya watu wale kabla. Alikumbuka kifo cha Mzee Mirambo na familia yake na mauaji ya watu wengine kadhaa.

Daniel alikuwa anatambua vizuri uwezo wa Mzee Mirambo kimapigano. Alikumbuka mstuko alioupata aliposikia Mzee Mirambo ameuwawa kikatili. Alihisi itakuwa Mzee Mirambo kagundua kitu cha siri kilichoyagharimu maisha yake.

Aliamua uchunguzi wake kuanzia kwenye nyumba za marehemu wote. Aliamua kuanza kwenye nyumba ya Mzee Mirambo kesho yake asubuhi.



Ilikuwa siku ya jumatano. Mji wa Masoko ukiwa na manyunyu ya mvua. Daniel alitoka kwenye ile nyumba ya kulala wageni. Kwa kutumia miguu alikuwa anaelekea mtaa wa Lumumba. Nyumbani kwa marehemu Mzee Mirambo.

Aligonga mlango taratibu. Akasikia sauti za hatua za mtu zikija mlangoni. Mlango ukafunguliwa. Daniel alifunguliwa mlango na kijana mmoja. Kiumri alikuwa kati ya miaka 20 na 30.

Baada ya salamu na utambulisho,Daniel alikaribishwa ndani.



“Naitwa Afande Daniel” Daniel alijatambulisha huku akionesha kitambulisho.



“Naitwa Kelvin”



“Una uhusiano gani mzee Mirambo?”



“Alikuwa kaka yangu”



“Wakati mauaji yanatokea wewe ulikuwepo ?”



“Hapana, nilikuwa safarini Mtwara”

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Uliongea na kaka yako mchana wa tukio ?”



“Ndio niliongea nae”



“Alikuwa katika hali gani?”



“Nilivyoongea nae alinambia ameenda Kisiwani kumwangalia mwanae”



“Kuwa na hali gani namaanisha alikuwa na huzuni au furaha?”



“Alikuwa kawaida tu”



“Nani unahisi itakuwa kamuuwa kaka yako?”



“Sifahamu afande”



“Nani alikuwa adui mkubwa wa kaka yako?”



‘Siwajui”



“Sawa nashukuru kwa ushirikiano wako”



“Ahsante”



Baada ya mahojiano na Kelvin ndugu wa marehemu Mzee Mirambo. Daniel alienda Mkumilu. Nyumbani kwa marehemu Edwin.

Katika nyumba hii Daniel alikutana na watu wengi kidogo.

Baada ya utambulisho Daniel aliomba kuongea na mchumba wa marehemu.

mchumba wa marehemu Edwin.



“Naitwa Afande Daniel”



“Naitwa Evelyne”



“Uliwasiliana na mchumba wako mchana kabla hajauwawa?”



“Ndio”



“Muliongea nini?”



“Alinambia amepewa kazi na anataka kwenda Kisiwani”



“Halafu ?”



“Nilimuuliza kazi gani hakunambia”



“Alienda Kisiwani?i”



“Sifahamu maana baada ya hapo simu yake haikupatikana tena”



“Unahisi nani itakuwa kamuua mchumba wako?”



“Mimi sifahamu afande” Akaanza kulia.



“Sawa,pole sana”



“Ahsante” Huku akijifuta machozi kwa kanga yake.



“Kuna kitu huko Kisiwani" Daniel alijisemea mwenyewe huku akiondoka.



Uchunguzi wake wa awali ulimuonesha lazima aende Kisiwani haraka iwezekanavyo.



"Kwanini marehemu wote kabla ya kufa Kilwa Kisiwani ilitajwa?" Alijiuliza mwenyewe, hakuwa na jibu. Ilimlazimu kwenda Kisiwani kupata majibu ya swali hili.



Usiku wa saa nne, Daniel alikuwa ndani ya boti ya kukodi, akielekea Kilwa Kisiwani kutafuta majibu ya maswali yake.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"..Mimi nina wasiwasi sana na huyu Bosi wa pale juu. Juzi alinionesha picha ya yule Mzee na jana amekutwa ameuwawa " Daniel alinasa kitu alichokihitaji. Kijana aliyekuwa msemaji mkuu katika genge lile alikuwa ni yule kijana Bosi Lee na kundi lake walimuonesha picha, na yeye aliwaelekeza shule anayosoma mtoto wa Mzee Mirambo na kupewa ujira wa shilingi elfu kumi.Aliitaja ile nyumba ya Lee huku akionesha kidole.



***



Kule ndani ya nyumba ilikuwa starehe sana kwa BosI Lee na kundi lake. Kulikuwa na tafrija kubwa ndani ya nyumba ile. Tafrija ya kufurahia ushindi.Ingawa Walikuwa hawajamtia mikononi Daniel Mwaseba lakini kufanikiwa kumuua Mzee Mirambo na kumkamata mateka Inspekta Nyange yalikuwa mafanikio makubwa sana kwao. Walikuwa wanakunywa kila aina ya pombe. Kulikuwa na nyama za porini za kutosha, wenye kupenda wanawake walikuwepo wa kutosha. Ilikuwa burudani na starehe kwao.



Ndani ya chumba kidogo ndani ya nyumba ile iliyosheheni burudani kulikuwa na mtu ambaye alikuwa kwenye mateso makubwa sana. Alikuwa amedhoofika mwili kama mgonjwa wa ukimwi. Mchana wake mtu huyu alipitia kwenye mateso makubwa sana. Kushindwa kujibu maswali mawili kulifanya aendelee kuteswa ndani ya Nyumba ile.



"Nani amekwambia kama nyumba hii kuna mpango wa siri na yuko wapi Daniel Mwaseba?". Inspekta Nyange alishindwa kujibu majibu ya kuwaridhisha watekaji. Kulifanya ajute kuisogelea nyumba ile.

Alipigwa sana Inspekta Nyange. Alichomwa na maji yanayodondoka kwenye mshumaa. Aliunguzwa kwa maji ya moto. Alifinywa na koleo sehemu za mapajani. Siku moja tu ilimwacha Inspekta Nyange amekonda vibaya sana. Hakika alikutana mtesaji anayejua kutesa. Aliachwa kwenye chumba cha mateso akiwa hana fahamu.



***



Daniel Mwaseba sasa alisogea karibu na nyumba ya maadui. Alikuwa amepanga afanye utafiti kwanza kuujua uwezo wa maadui halafu akajipange ili arudi na nguvu mpya kuja kukata mzizi wa fitna.



Ghafla kule ndani katikakati ya sherehe runinga ya Bosi Lee ilimuonesha waziwazi Daniel Mwaseba akiisogelea Nyumba yao..Runinga ya Bosi ilikuwa imehamishiwa katika ukumbi wa sherehe. Watu wote ukumbini walimshuhudia Daniel akinyatia.



"Yes ni Daniel Mwaseba, kajileta mwenyewe sasa sherehe yetu itafana zaidi" Lee aliropoka kwa nguvu huku akipiga ngumi ya nguvu ya mkono wa kulia katika kiganja cha mkono wa kushoto. Kumpata Daniel ilikuwa ushindi mkubwa kwake, maana Daniel kilikuwa ndio kikwazo kilichobaki, na sasa bila kutumia nguvu Daniel alijileta mwenyewe mikononi kwa Bosi Lee.



Sasa sherehe ilisimama ghafla. Wana sherehe wote waligeuka kuwa watazamaji wa runinga. Waliokuwa wamewahi kusikia habari za Daniel walikuwa na hofu moyoni kwao. Ila wasiozisikia habari zake walihisi ni kama kidudu mtu tu akikinyatia kifo chake mwenyewe.



Daniel aliichunguza kwa makini Nyumba ile na kupata alichokuwa anakitaka. Alikuwa anahitaji sehemu rahisi ya kuingilia ndani ya Nyumba ile na pakutokea. Akarudi nyuma kwenda kujipanga kwa shughuli mzito kesho yake.



Watazamaji wa runinga sasa walikuwa katika mshangao, picha ya mnyatiaji haikuwa inaonekana tena. Iliyeyuka katika upeo wa macho yao. Daniel aliyeyuka katika kioo cha runinga ile. Sasa Ilikuwa patashika ndani ya nyumba.

Lee alichelewa kutuma watu kwenda kumkamata Daniel. Alikuwa anatarajia minyatio ya Daniel ingemfikisha karibu na mdomo wake hatari, mdomo wa mamba. Ila sasa alikuwa katika majuto makuu. Subira ilimponza. Alifanya makosa kwa kutegemea Daniel atafanya kosa kama alilofanya Inspekta Nyange. La kujileta mwenyewe bila tahadhari. Daniel Mwaseba hakuwa mtu wa aina hiyo. Daniel alipotea!



Wakati Lee akituma watu wake kwenda kumtafuta. Daniel alikuwa ndani ya boti akirejea Masoko kujipanga vizuri kuja kuisambaratisha ngome ile.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Ndani ya nyumba ile, sherehe iligeuka shubiri. Sasa ilizuka kazi ya dharura ya kumtafuta Daniel popote alipo, Yaani ilikuwa ni msake mpaka umpate!



Boti zaidi ya kumi zilikuwa baharini zikimtafuta Daniel. Watu hamsini walijigawa makundi ya watu wawiliwawili. Walikuwa wanatafuta kila sehemu ndani ya Kisiwa kile. Wengine walibaki kambini kulinda kambi yao na kumlinda mateka wao, Inspekta Nyange.

Aliulizwa kila mtu ndani ya kisiwa kile, hakuna aliyekuwa na jibu kueleza wapi alipo Daniel. Wala hawakuwa wanamfamu Daniel. Ingawa walitumia na picha zake katika kumtafuta waliambulia patupu. Daniel aliyeyuka mithili ya mzimu!



Kosa la Lee lilikuwa kuchelewa kutoa maamuzi baada ya kuona Daniel haonekani kwenye ile runinga ya kijasusi. Kipindi wao wanaingiza boti zao baharini kumsaka Daniel. Yeye alikuwa upande wa pili wa bahari akishuka kwa madaha ndani ya boti. Nahodha wa boti lile kwa bahati mbaya hakupata abiria mwengine wa kumpeleka Kisiwani. Hiyo ilikuwa bahati mbaya kwa Lee na kundi lake pia. Maana labda angerudi wangekutana nae na kumuuliza kama alimuona au kumpakia Daniel. Wakati kwa upande wa Daniel ilikuwa moja ya faida kubwa sana.



Ndani ya dakika ishirini Daniel hakuonekana ndani ya Kisiwa. Lee akaona hatari inamkaribia sasa. Alipandwa na hasira sana.

Hii wiki Ilikuwa ngumu sana tangu waanze mchezo huu mchafu! Wiki ya misukosuko na hekaheka.

Lee akawa anaenda katika chumba cha mateso kumalizia hasira zake kwa Inspekta Nyange, mpaka sasa alikuwa ameshatuma watu wake aliowaamini thelathini kwenda Masoko kumsaka Daniel. Miongoni mwa watu hao Kishoka alikuwemo. Aliwapa maagizo mawili, warudi na kichwa pamoja na utumbo wa Daniel kabla hakujapambazuka!

Kundi la watu thelathini, wauaji waliobobea likatua ndani ya Masoko ndani ya saa saba za usiku.

Walikuwa na jukumu la kupeleka kichwa na utumbo kwa Daniel. Kiwiliwili wataamua wao watakifanya nini. Huu haukuwa utani. Yalikuwa ni maagizo au tunaweza ita amri toka kwa Lee. Ilikuwa ni lazima wapeleke utumbo na kichwa kwa Bosi Lee kabla hakujapambazuka...

Lee alikuwa na hasira sana. Hakutegemea kuponyokwa na Daniel kirahisi vile. Aliamua kupunguza hasira zake kwa kwenda kumtesa inspekta Nyange. Kutesa ndio ilikuwa starehe yake kipindi anapokuwa na msongo wa mawazo kama ule.

Alimkuta inspekta Nyange bado hajarejewa na fahamu. Alitoka Lee alielekea jikoni. Alirudi na ndoo ya maji kubwa. Alimmwagia Inspekta Nyange ile ndoo ya maji. Inspekta Nyange aliamka taratibu toka kuzimu. Angejua alichorudishiwa duniani bora angelala kule kule kuzimu!

Alivyoamka alikutana na Lee. Sura yake ilifanana kabisa na roho yake!



Lee alichukua gundi aina ya 'super glue'. Alimpaka kwenye macho. Halafu akamfumbisha macho kwa mikono. Baada ya dakika kumi alimuachia. Macho ya Inspekta Nyange yaliganda. Hakuwa anaweza kufungua macho tena!



Lee akaanza kumvuta Inspekta Nyange kwenye macho. Kwa nguvu..Maumivu akiyoyasikia Inspekta Nyange hayana mfano. Lee akaona haitoshi alichukua kiberiti na kuwasha njiti moja. Akawa anamchoma pale machoni kwenye gundi. Nia yake ni kulainisha ile gundi. Inspekta Nyange alilia sana. Aliteseka sana. Machozi hayakumtoka lakini.Yatatoka vipi ilhali macho yamezibwa? Kilio cha Inspekta Nyange ilikuwa faraja kwa Lee. Alisahau kwa muda habari za Daniel.

Alichukua kiwembe na kumchana machoni Inspekta Nyange, nia ni kumrudisha katika hali ya kawaida.Sasa hakuwa anasikia raha kutesa bila mtesaji kumwona anayemtesa.Alimchanachana vibaya sana.Damu zilimwagika nyingi sana. Alikuwa kama anamperesheni bila ganzi!

Wakati anaendelea kumpasua Bosi Lee alisikia kitu cha baridi kimemgusa shingoni. Hakuwa na haja ya kuambiwa nini kilimgusa. Aliguswa na mdomo wa Bastola shingoni mwake. Lee alistuka sana, hakutegemea kitendo kama kile kutokea katika himaya yake. Alipogeuka nyuma bastola sasa ilitazamana na utosi wake. Macho yake yalimuona vizuri sana. Alikuwa ni Daniel Mwaseba !



E bwana wee!!!





Wakati anaendelea kumpasua Bosi Lee alisikia kitu cha baridi kimemgusa shingoni. Hakuwa na haja ya kuambiwa nini kilimgusa. Aliguswa na mdomo wa Bastola shingoni mwake. Lee alistuka sana, hakutegemea kitendo kama kile kutokea katika himaya yake. Alipogeuka nyuma bastola sasa ilitazamana na utosi wake. Macho yake yalimuona vizuri sana.

Alikuwa ni Daniel Mwaseba !



Sasa Lee alitekwa na Daniel Mwaseba. Daniel akiwa makini alimwangalia Lee kwa jicho moja huku jicho lengine akimwangalia aliyekuwa mateka wa Lee. Lakini hakumtambua. Sura yote ya mateka ilitapakaa damu. Alikuwa na vidonda mwili mzima. Amedhohofika sana.

Kumbe Daniel alivyoondoka alipofika Masoko alibadilisha maamuzi.



"Liwezekanalo leo lisingoje kesho" Alikumbuka msemo wa mwalimu wake akiwa Depo kule Moshi. Lakini kutokana na ulinzi aliouona ilimbidi aongeze nguvu. Sasa alirudi kazini akiwa na askari ishirini, yeye akiwa ndio kiongozi wao.

Alikuja na askari waliokuwa wameiva. Makini katika kazi yao.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Ndani ya dakika kumi na tano waliisambaratisha kambi ya Lee. Waliacha walinzi wote wamelala katika kambi ile. Huku askari watano aliokuja nao Daniel nao walikuwa wameuwawa. Ulikuwa mpambano wa kimyakimya huko nje. Wakati Lee anapambana na mwili dhaifu wa Inspekta Nyange. Huko nje Daniel na askari wenzie wakipambana na miili imara ya walinzi wa Lee. Hakukuwa na mtu akiyaangalia runinga kuuona ujaji wa askari wale. Walijisahau!

Sasa Lee alikuwa mikononi mwa Daniel Mwaseba. Waliongezeka askari wawili waliubeba mwili wa Inspekta Nyange. Wakati wanatoka nje ya Nyumba ile Lee alisikitika sana. Daniel aliacha maafa makubwa katika nyumba ile. Walikuwa wanatembea juu ya maiti na madimbwi ya damu!



ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog