Search This Blog

Saturday 5 November 2022

MAPIGO YA MOYO - 1

 






IMEANDIKWA NA : HAKIKA JONATHAN



*********************************************************************************



Simulizi : Mapigo Ya Moyo

Sehemu Ya Kwanza (1)



Nikiwa sijitambui nilishituka usingizini na kuanza kupiga kelele kuomba msaada, sikuamini nilichokiona kwani mwili wangu ulijaa vidonda kila sehemu ya mwili wangu. Maumivu makali yaliutesa mwili wangu na kunikosesha furaha nafsini mwangu.



Sehemu zote za mwili wangu zenye vidonda zilifungwa kwa bandeji na kunifanya nizidi kuwa na hofu ,kwani sikujua chanzo chochote cha majeraha yale .Nilijalibu kuangaza kila kona ya chumba kile ili niweze kupata msaada, lakini niliambulia halufu kali ya dawa iliyopenya vilivyo puani mwangu na kunifanya nipige chafya mfululizo.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Chembechembe nyekundu za damu zilitoka mdomoni mwangu na kuchafua shuka jeupe nililokuwa nimejifunika, kutokana na chafya yangu isiyokuwa ya kawaida kwa mtu mwenye afya njema. Nilianza kulia kama mtoto mdogo aliyenyimwa ziwa na mama yake, baada ya kugundua sitoweza kutembea tena kwani miguu yangu ilikua imekatwa.



Nikiwa na huzuni niliyashika magoti yangu yaliyofungwa na bandeji, ghafla maumivu makali yaliongezeka mwilini mwangu kwani nilitonesha vidonda ambavyo vilikuwa bado vibichi na kujikuta nikianza kutokwa na machozi kama mtoto mdogo.



"Mungu wangu!! " ,ilisikika sauti ya mshangao kutoka kwa msichana mrembo aliyevalia mashati meupe, bila shaka alikuwa ni nesi wa hospitali ile. Alitembea halaka sana kuelekea kitandani kwangu ili aweze kunipatia msaada.



"Pole sana kaka yangu, nakuomba upunguze jazba kwasababu unatonesha vidonda vyako na kujiongezea maumivu. "Alizungumza nesi yule kwa sauti ya upole iliyojaa huluma huku akiandaa sindano ya usingizi ili anichome nipate kulala.



"Asante sana dada yangu, lakini nimefikaje hapa? Nimepatwa na nini?,Hii ni hospitali gani?, na kwanini mmenikata miguu yangu?



Niliuliza maswali mengi mfululizo huku nikiwa na simanzi kubwa kupoteza miguu yangu, na kupoteza kumbukumbu yangu kichwani.Sikuweza kutambua chochote kwa wakati ule hata jina langu sikuweza kulitambua.



"Ulifikishwa hapa juzi ukiwa umepoteza fahamu, mwili wako ulijaa vidonda kila sehemu huku miguu yako ikiwa imesagika yote miwili. Kutokana na taarifa tuliyopewa ulikuwa umepata ajari ya gari. "



Msichana yule alinipatia majibu ya maswali yangu na kunifanya nizidi kupatwa na mshangao, "Nani alinifikisha hapa?, niliweza kuuliza swali lingine ili kupunguza maswali mengi yasiyo na majibu yaliyoko kichwani mwangu.



"Msichana aliyekugonga na gari kwa bahati mbaya, ndiye aliyekufikisha katika hospitali hii ya taifa ya Muhimbili kitengo cha mifupa MOI. Binti huyu alijitambulisha kwa jina la Jesca Jonathan, na kutokana na ripoti ya daktari miguu yako ilitakiwa kukatwa halaka sana ili kuokoa maisha yako.



Yalikuwa maelezo marefu sana kutoka kwa nesi huku machozi yakimtoka, kutokana na huluma iliyomjaa hasa akinitazama na hali mbaya niliyokuwa nayo.



*****************



Nesi alinichoma sindano ya usingizi na kujikuta nikilala usingizi mzito ulionipelekea kusahau maumivu niliyoyapata kwa wakati ule. Nilikuja kuzinduka siku inayofuata na kushangazwa na kile nilichokuwa nakiona mbele yangu.



Msichana mrembo aliyekuwa chanzo cha maisha yangu kuharibika, alikuwa amesimama pembeni ya kitanda changu akiwa pamoja na nesi aliyekuwa akinihudumia. Hasira na chuki vilinitawala dhidi ya msichana yule na kujikuta nikitamani kumtoa roho yake kama ingiwezekana,kwani sikuona thamani ya yeye kuwepo hapa duniani.



"Kaka huyu ndiye dada aliyekugonga na gari kwa bahati mbaya na kukufikisha hapa hospitalini kwa matibabu", nesi alizungumza maneno makali yaliyopenya maskioni mwangu na kuuchoma moyo wangu mithili ya mtu akanyagapo kaa la moto bila kutambua.



"Pole sana Robert, nafahamu kuwa unaumia sana kwa matatizo haya niliyokusababishia. Lakini haikuwa makusudio yangu kukusababishia ulema huu bali ni ajari tu ambayo ilitokea kwa bahati mbaya ",. msichana mrembo na mtoto wa kitajiri Rose alizungumza maneno ya kuniomba msamaha huku nesi akipigwa na butwaa kwani hakufahamu chochote kuhusu kufahamiana kwetu mimi na msichana yule.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Mimi kwa wakati ule nilizidi kulia kwa uchungu kwani niliamini Rose kanigonga na gari kwa makusudi, kwani nilikua kikwazo kikubwa katika mapenzi yake na mtoto wa raisi. "Nisamehe Robert, nisamehe Robert!...niko tayali kuwa na wewe. Nimeamini unanipenda kwa dhati Robert ",..Rose alizungumza maneno hayo huku akilia mithili ya mtu aliapo msibani, mala baada ya kufiwa na mtu tegemezi katika maisha yake.



"Siwezi kukusamehe mnafki kama wewe,pia baba yako mzee Jastini kapoteza maisha ya wazazi wangu na kila niliyemtegemea ili tu nisiweze kuwa karibu na wewe na niache kukufuatilia " ,niliropoka maneno kwa jazba na sauti kubwa iliyomfanya kila mgonjwa aliyekuwa wodini amelala kukurupuka na kutazama kilichokuwa kikitokea kwa wakati ule.



Nesi ilibidi asimamishe mazungumzo yetu,kwani yalikuwa kero kubwa kwa wagonjwa na wahudumu wa hospitali ile ya taifa ya Muhimbili. "Sa, sa.. ma... hani Rose na...na.. omba mpunguze kelele kwani mnawakera wagonjwa wengne " ,.Nesi alizungumza kwa kusitasita kutokana na woga aliokuwa nao mala baada ya kumtambua Jesca Jonathan jina lake halisi ni Rose, mtoto wa mfanyabiashara maarufu na katili nchini Tanzania. Umaarufu pia wa familia ya mzee Jastini uliongezeka pale Rose alipotakiwa kuolewa na mtoto wa Raisi aliyeitwa Jacob.



Ilibidi tukae kimya kwani wote tulikuwa tukilia kwa wakati ule,nilifuta machozi huku nikishika magoti yangu na kusononeka kukosa miguu yangu iliyo kwisha katwa. Rose aliigundua huzuni yangu ilibidi anisogelee na kunikumbatia ili kunifariji na kunitia moyo, kitendo nilichokiona kama unafki kwangu.



Rose alizidi kunibembeleza na kunitia moyo katika siku zote nilizokuwa nikipatiwa matibabu mpaka majeraha yangu yalipopona kabisa."Kesho mgonjwa wako tutampatia ruhusa kwani afya yake imerudi katika hali ya kawaida ",dokta alimpatia ujumbe Rose kuhusu afya yangu na kutufanya tuwe na furaha sana kwa wakati ule. ",Asante sana dokta kwa kumuhudumia vizuri mgonjwa wangu"Rose alimshukuru dokta na kumpatia bunda la pesa kama shukrani kwa kunihudumia vizuri.





Siku iliyofuata niliweza kupatiwa ruhusa kurudi nyumbani, japo nilikuwa na furaha afya yangu kurudi katika hali ya kawaida lakini sikuweza kujuwa hatima ya maisha yangu. ",Robert mpenzi wangu nakupenda sana, sikujua kama ulikuwa unanipenda kwa dhati kiasi hiki ".Rose alizungumza maneno haya kwa tabasamu na kufanya uzuri wake kuonekana vyema katika mboni ya macho yangu. "Nakupenda pia Rose lakini siko tayali kuwa na wewe, nimeteseka sana kulitafuta penzi lako kwa muda mrefu na kuambulia maumivu.....inatosha siko tayali kuendelea kuumia ",nilizungumza kwa huzuni kubwa huku Rose akinifuta machozi na kunikumbatia.



"Kwa sasa nataka kufunga ndoa na wewe, sitaki tena kuolewa na mtoto wa raisi ",Rose alininyenyua na kuniweka kwenye baiskeli ya walemavu wa miguu aliyoninunulia na kisha kunitamkia maneno mazito yaliyonitia hofu sana. "Baba yako ataniua Rose mimi siko tayali, kawaua ndugu zangu na wazazi wangu ili nisiwe na wewe.... Siko tayali Rose.... Sitaki tena kuumia ",nilimjibu Rose majibu makali huku nikikumbuka vifo vya wazazi wangu walivyouawa kikatili kwa kuungua na moto baada ya banda letu la makuti kuchomwa na majambazi waliokuwa wametumwa na mzee Jastini kuniangamiza mimi na familia yangu. Nilikumbuka jinsi nilivyoshuhudia maiti saba zilizoungua na kuharibika vibaya, maiti mbili zilikuwa za wazazi wangu na zingine za wadogo zangu.Huku mimi nikiponea chupuchupu kwani siku hiyo nililala Morogoro mjini,nilipoenda kutafuta kazi baada ya kumaliza chuo kikuu.



Niliendelea kukumbuka jinsi kijiji chetu cha Mikese walivyohuzunika kutokana na msiba uliyoikumba familia yetu, huku wakinidharau baada ya kugundua kuwa kumtaka Rose binti wa kitajiri kimapenzi ndio chanzo cha vifo vya wazazi wangu. ",Watoto wetu wakisoma hawataki kuoa nyumbani kwao, hawataki kuoa masikini wenzao.... Ona sasa madhara yake " ,nilikumbuka sauti ya mzee mmoja aliyeropoka maneno hayo msibani wakati tukiaga mwili wa ndugu zangu.



"Rose siwezi kuwa na wewe..... Umeniumiza sana ",nilitamka maneno hayo kwa msisitizo baada ya kukumbuka matukio ya nyuma yaliyotokea na kubadilisha furaha ya maisha yangu, huku chanzo kikiwa mimi kumpenda Rose msichana niliyesoma nae chuo kikuu cha SUA na kushindwa kuheshimu hisia zangu kutokana na umaskini wangu niliokuwa nao.



"Robert kila kitu kiko tayali, kesho inatakiwa mimi na wewe tufunge ndoa uwanja wa taifa....Jacob kaniruhusu nifunge ndoa na wewe badala yake kwani kagundua kuwa unanipenda sana tena kwa dhati ".....Rose alizungumza maneno yaliyonitia moyo na kunifanya nikubaliane naye. ",What....!! unasema kweli?...... niliongea kwa mshangao huku nikifuta machozi yangu na kukaa vizuri kwenye kibeskeli changu ili nimskie vizuri., "Ndio.... Kesho Tanzania nzima wanajua mimi nafunga ndoa na Jacob mtoto wa raisi, kwahyo kesho muda wa harusi utatokea wewe badala yake. "Rose alisisitiza huku akinitaka kukubaliana naye jambo ambalo sikuweza kulipinga tena kwa wakati ule.



Hatimae siku iliwadia, maelfu ya wananchi walifika uwanja wa taifa kushuhudia mtoto wa raisi akifunga ndoa. Wageni mbalimbali kutoka nchi jirani walifika kushuhudia sherehe hiyo, "Watakapo ita bwana harusi, tutaenda wote kwa pamoja lakini wewe utakua kama msindikizaji wangu ili wasigundue chochote ",Jacob alinipa maelekezo huku mimi nikimshangaa tu kwani ilikua mala ya kwanza kukutana naye dhaidi ya kupata taarifa zake kutoka kwa Rose.



"Ndugu wananchi tunaomba mpige kelele za shangwe bwana harusi anapoingia uwanjani ",MC alizungumza huku shangwe zikifuatia huku Jacob akisukuma kibaiskeli changu cha magurudumu matatu tukielekea uwanjani alipoketi bibi harusi. Shangwe na nderemo zilipungua kadri tulivyokuwa tukikalibia uwanja kwani walishangazwa na muonekano wetu .



Maelfu ya watu walikaa kimya huku wakishangaa kile kilichokua kinatokea kwa wakati ule, "Namuomba bwana harusi amvalishe pete bibi harusi " ,Mchungaji aliongea huku akiwa hajui kati ya mtoto wa raisi bwana Jacob na mimi, ni nani kati yetu alikuwa anahusika na ndoa ile kutokana na muonekano wetu kufanana kwa kila kitu ……huku pia kukiwa na tetesi za Jacob kutohusika na ndoa hiyo.



…………………………………http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



"Sniper" (mlenga shabaha) akiwa anajiweka tayali kwa kunifyatulia risasi aliendelea kujiweka tayali huku akisubilia kushuhudia kati yangu na Jacob ni nani alikuwa muhusika wa ndoa ile. "Leo ni mwisho wako mpuuzi wewe, nimekuonya sana hutaki kunisikia ", baba yake Rose alizungumza kwa sauti ya chini sana huku akiangalia juu kabisa ya uwanja uelekeo ambapo mlenga shabaha alipo kwa ajili ya kutekeleza mauaji yangu.



Mzee Jastini aliamua kuandaa mtu kwa ajili ya kuniua kutokana na tetesi alizozisikia kuwa, kuna mipango ya siri iliandaliwa ili mimi nifanikiwe kumuoa Rose."Sitaki aibu, Kijana huyu fukara hawezi kumuoa mwanangu ……nitaiweka wapi sura yangu?? ……mungu wangu kashakua kilema, na ulema huo ndo kabisaaa nitaaibika zaidi siwezi mruhusu amuoe binti yangu labda niwe nimekufa " mzee Jastini aliongea huku akiwa amepaniki na kutoka sehemu waliyokuwa wameketi wageni rasmi, baada ya kushuhudia nikiingia uwanjani huku Jacob akiskuma kibeskeli changu. "Nimeamini hapa kuna kitu siyo bure, ngoja nimkomeshe kijana huyu kabla mambo hayajaharibika ",mzee Jastini alielekea faraghani na kumpigia moja ya vijana wake aliowatumia katika kutekeleza matukio mbalimbali ya mauaji ili ajaribu kuniua kwa mara nyingine tena.



…………………………………



"Paaaaaah, paaah ……paaah "mlio wa risasi tatu zilizopigwa mfululizo ulisikika na kujikuta nikiishiwa nguvu na kudondoka chini mara nilipotoa pete mfukoni na kumvalisha Rose katika kidole chake. "Jacob my son don't die " ,( mwanangu Jacob usife) niliiskia sauti ya mheshimiwa raisi kwa mbali sana akimsihi mwanae asife japo alikuwa tayali ameshachelewa, Jacob aliamua kunikinga na risasi baada ya kushuhudia nikipigwa risasi ya kwanza tumboni."Aaaaah ……"Jacob alipiga kelele na kisha kupoteza maisha baada ya kupigwa risasi mbili kifuani huku akiwa amenikumbatia.



"Robert usife Robert, Jacob rudi Jacob ……fumbua macho angalau uniage……hukustahili kifo hiki Jacob ,bora ningekufa mimi wewe huna hatia. Rudi Jacob rudi ……" sauti ya huzuni ilisikika kutoka kwa Rose, huku akiwa ameshikilia miili ya watu wawili katika mikono yake.



…………………………………



Askari waliendelea kuzunguka kila kona ili kumnasa muhusika wa mauaji ya Robert na kunijeruhi vibaya,huku wakishirikiana na wananchi walioshuhudia tukio lile. "Unatakiwa uondoke Dar es salaam haraka iwezekanavyo kabla hujakamatwa, kukamatwa kwako kutaniweka sana matatizoni ",bwana Jastini alimsihi kijana wake aliyehusika na shambulio lile, wakiwa ndani ya gari kuelekea katika maficho yao ya siri yaliyoko nje ya mji.



Baada ya jambazi yule kutekeleza shambulio lile, aliiacha bunduki ile aina ya Semi_automatic machine gun (smg) mahali pale, na kisha kujichanganya katikati ya watu waliokuwa wakikimbia bila utaratibu ili kuokoa maisha yao. Jambazi hili lilitoroka kirahisi na kushindwa kukamatwa na askari na wala kujurikana hata sura yake.



"Aliyehusika na haya yote lazma atalipia, "raisi aliongea huku akinitazama nikipatiwa matibabu na kutolewa risasi, machoni alionekana kuwa na huzuni sana huku hasira ikiipamba sura yake kutokana na mwanae kupoteza maisha na muuaji kushindwa kufahamika.



Raisi akiwa ikulu, hakuweza kulala kabisa!, alitembea huku, mala akaenda kule, alilala akakosa usingizi, hakuwa na jinsi zaidi ya kuamka na kwenda kuketi sebuleni. "Lakini, hapa kuna kitu, nahisi mzee Jastin atakua anasiri nzito kaificha, kwanini alionekana kuwa na wasiwasi sana alipomuona Robert?, kwanini alitoweka bila hata kuaga baada ya mauaji ya mwanangu na mpaka sasa hajanipigia simu? ",raisi wa Tanzania, raisi aliyekuwa kipenzi cha watu kutokana na uongozi wake kuwa wa haki na kuleta maendeleo mazuri kwa wananchi, akiwa ameketi sebuleni aliendelea kujiuliza maswali mengi kichwani bila kupata jibu.



"Kesho nitamtembelea tena Robert hospitalini, lazima atakuwa anafahamu chochote ",raisi aliinuka na kisha kuelekea chumbani kwake huku akiongea peke yake mithili ya kichaa na kuamua kunitembelea hospitalini siku iliyofuata.



9;00 asubuhi.

Ilikua siku ya jumanne, siwezi kuisahau siku hiyo kwani ni moja ya siku ambazo niliweza kuamini kuwa mwenye pesa si mwenzako! ,japokuwa niliapa sitoweza kuzungumza chochote kuhusu kifo cha Jacob, nilijikuta nikizungumza kila kitu bila kuacha hata nukta !



" Nimefanya nini sasa, Rose atanifikiliaje? ,si alinikataza nisiseme chochote kwani baba yake ataweza kuwa hatarini? ",nilikuwa nikijilaumu huku nikijuta kumwambia ukweli raisi, baada ya kunitembelea muda mfupi uliopita.Nilijiona mwenye makosa japokuwa mzee Jastini alikuwa amenitendea mambo mengi mabaya sana ambayo hakuna binadamu yoyote angeweza kumsamehe kama angeweza kutendewa.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

*******************



Ilikuwa ni asubuhi mida ya saa mbili siku ya jumanne, nikiwa nimeketi kitandani nilishangaa kuona madaktari wakikimbia huku na kule ndani ya wodi niliyokuwa nimelazwa.



"Mmmh hapa kuna jambo sio bure ",nilizungumza peke yangu huku nikiwashangaa madaktari ambao walionekana kuzunguka ndani ya wodi kukagua hali za wagonjwa huku manesi wakifanya usafi na wengine kubadili mashuka ya wagonjwa yaliyokuwa machafu, na kutandika mashuka masafi.



"Samahani wewe ndiye Robert!,"nilijikuta nikiulizwa swali na nesi ambaye sikuwahi kumuona tangu jumamosi nilipopigwa risasi na kufikishwa katika hospitali ya Muhimbili, hospitali ambayo ilikua mala yangu ya pili kupatiwa matibabu huku nikiwa nasumbuliwa na matatizo yanayotaka kufanana.



"Ndiye mimi ",nilimjibu nesi, na kuanza kumshangaa sana kwani aliniomba nimpishe kitandani mala moja. Bila shaka!,nilitii ombi lake na haraka sana nilimuona akitandika kitanda changu kwa shuka jeupe, na kutoa shuka ambalo nilililalia kwa siku tatu mfululizo huku likiwa na mabaka mabaka ya damu kutokana na jeraha la risasi nililokuwa nalo.



Baada ya nesi yule kumaliza kutandika, aliweza kuondoka na kisha niliweza kurudi kitandani kujilaza huku nikiwaza kuhusu hatima ya mapenzi yangu ya mateso, na kujuta kumpenda Rose kwani majanga hayakuisha hata siku moja katika maisha yangu.



"Kijana hujambo ……!,unaendeleaje? lilikuwa ni swali kutoka kwa raisi, raisi ambaye alifika wodini bila mimi kutambua kwani nilikuwa na mawazo mengi kwa wakati ule, nikiwaza kuhusu hatima ya maisha yangu yenye vitimbwi kila kukicha.



Haraka nilikurupuka kutoka kwenye dimbwi la mawazo, na kisha kumsikiliza raisi alichokuwa akikizungumza huku nikipata jibu la swali ambalo nilijiuliza kuhusu pilika pilika za madaktari na manesi walizokuwa nazo asubuhi ile.



"Naendelea vizuri mheshimiwa ",nilimjibu raisi huku nikijilazimisha kuficha huzuni na mawazo mengi niliyokuwa nayo.



"Sasa nataka unisaidie kitu, pesa hii hapa, niambie kuna nini wewe na mzee Jastini mbona alitaka kukuua ",raisi aliongea kwa kunitega ili aweze kujiaminisha kama kweli kitu alichokiwaza kilikua sahihi.



Kutokana na pesa nyingi nilizokuwa nimeoneshwa, pesa ambazo zilikuwa ndani ya briefcase jeusi, sikuwa na jinsi ilibidi nitiririke kila kitu. Kwani njaa nayo ilikuwa ikinisumbua, sikuwa na kazi zaidi ya kumtegemea Rose ambaye alikuwa kama tegemezi langu lililobakia.



"Nilimpenda Rose tangu chuoni lakin alinikataa kwa sababu nilikua masikini, kama mwanaume mwenye mapenzi ya dhati sikukata tamaa, niliendelea kumfuatilia Rose hata baada ya kumaliza chuo, lakini Rose hakuwa tayali kunipenda hivyo basi aliamua kumwambia baba yake kuwa nilikua nikimfuatilia. Baba yake alinipatia onyo lakini sikujali, nilijikuta nikiendelea kumfuatilia Rose kitendo kilichopelekea wazazi wangu kuuawa na mzee Jastini ",niliamua kuishia hapo kwani nilisita kutamka jambo baya ambalo niliweza kufanyiwa na Rose, kuhusu kugongwa na gari na kisha kuvunjika miguu kwani sikujua kuwa alinigonga kwa makusudi au laa!



Baada ya kumalizia kumwelezea raisi kuhusu siri hii, aliamua kuondoka haraka na kisha kuniachia mawazo mengi sana kichwani huku nikijilaumu na kujuta kusema ukweli kwani Rose angeweza kunichukia na kisha kuniacha kwani nimemuweka baba yake mahali pabaya, lazima ataweza kukamatwa na kushtakiwa kuhusika na mauaji ya Jacob, mtoto wa Raisi.



Rodgers akiwa anaonekana kukosa amani kabisa kuliko siku zote ,alishindwa kula hata chakula kwani alipojalibu kula hamu ilikata ghafla hasa baada ya kukumbuka kosa ambalo ameweza kulifanya kwa bahati mbaya. "Shit! mission failed ………!",sijawahi kushindwa! lakini katika swala hili, nikizubaa lazima serikali itafanikiwa kunikamata.",ilikuwa ni sauti ya hasira kutoka kwa Rodgers, jasusi wa kimataifa ambaye aliongea huku akitupa simu yake chini na kuipasua ,kwani alikuwa na hasira iliyopitiliza kiasi kwamba angeweza kuua mtu yeyote kama angekuwa karibu naye.



"Vipi Rodgers kulikoni!, nimesikia sauti ya kitu kudondoka chini, una tatizo gani ",mzee Jastin alifika haraka sana sehemu ambayo ilikuwa imejaa zana mbalimbali za kufanyia mazoezi, bila shaka ukiingia tu lazima utatambua chumba kile kilikuwa ni cha kufanyia mazoezi, tena mazoezi ya karate na wala sio mbio za mita mia moja. Mzee Jastin alishangaa kumkuta Rodgers akiwa ana mawazo mengi, huku simu yake ikiwa imepasuka vipande! vipande! na kuamua kumuulza tatizo ambalo lilikuwa likimsumbua.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Bosi!, siku ambayo nafanya mauaji, nilishika siraha bila kuvaa gloves, bila shaka wataalamu wa kompyuta wanaweza kufahamu muuaji wa Jacob, kwasababu finger prints lazima zitaonekana tu! ",ilibidi Rodgers, jasusi wa kuaminika na mzee Jastin amweleze bosi wake ukweli. Taarifa ambayo ilimshtua sana mzee Jastin, kwani alitambua kuwa muda wowote lazima muuaji angeweza kutambulika!



"Big mistake! Lakini kulaumiana hakutasaidia chochote, inatakiwa haraka sana nikukatie tiketi ya ndege ukapunge upepo Mombasa, "mzee Jastin, mfanyabiashara maarufu na katili nchini Tanzania alizungumza huku akitafuta namba ya rafiki yake ambaye alikuwa akifanya kazi katika shirika la ndege la Air Tanzania.



"Tiketi imebaki moja ya leo usiku!, japokuwa watu wengi wanaitaka lakini mimi nakuuzia wewe rafiki yangu ………japokuwa uliniambia abiria wako ameahirisha safari ",ilikuwa ni sauti ya mtu aliyeonekana kuongea kwa upole sana, na ustaarabu wa hali ya juu moja ya sifa ambazo zilizingatiwa kwa wafanyakazi wa mashirika ya usafiri wa anga. Sifa zao za ukarimu hazikuachana mbali na wafanyakazi wa benki pamoja na kampuni mbalimbali za simu Sauti hiyo ilitoka kwa Juma, rafiki kipenzi wa mzee Jastin baada ya kupigiwa na rafiki yake aliyekuwa anahitaji tiketi ya ndege kuelekea Mombasa.



"Sasa hivi ni saa kumi jioni, ndege inaondoka saa mbili usiku jiandae! Kuanzia kesho jumatano maisha yako yatakuwa katika ngome yetu ya Mombasa, nenda kajifiche huko ",mzee Jastin alimpatia maelekezo Rodgers ,mala tu baada ya kukata simu ya Juma. Huku Rodgers akitabasamu na kisha kwenda kufungasha vilago vyake kujiandaa na safari.



*******************



"Baba ni muuaji, usijilaumu sana kusema ukweli, aliyokutendea yanatosha, ",Rose aliongea huku akinifuta machozi baada ya kumweleza kila kitu kilichokuwa kimetokea. Jinsi raisi alivyonitembelea na kunipatia pesa nyingi nimweleze chanzo cha ugomvi wake mimi na mzee Jastin..



"Nyamanza mpenzi!, let's go home ……just usimfikilie kabisa dady, baba gani siku ya nne sasa hajui mwanae anaishije, kazi tu kuvuruga mapenzi ya watu ",Rose alizidi kufoka huku akinipandisha katika baiskeli yangu ya mataili matatu kwani tayali tulikuwa tumeruhusiwa.,niweze kwenda nyumbani.



Rose alionekana kuwa na hasira sana kwani tangu baba yake alipotoweka siku ya tukio, mpaka natolewa hospitalini tulikuwa hatufahamu sehemu ambayo alikuwa ameelekea, huku Rose akiishi peke yake kwani hakuwa na mama wala wadogo zake, au ndugu yoyote aliyekuwa akiishi naye.



Siku zote Rose hakutambua ni kwanini alikuwa akilazimishwa na baba yake kuolewa na mtoto wa raisi, marehemu Jacob. Lakini siri haikuwa siri tena, aliweza kugundua kila kitu, mpaka biashara haramu ambazo baba yake mzee Jastin alikuwa akizifanya



"Mtoto wako akiolewa na raisi, bila shaka raisi atakuwa ndugu yako .kupitia wewe tutaingiza madawa mengi ya kulevya nchini Tanzania bila kuguswa na kujiingizia pesa ndefu sana " ,ulikuwa ni ujumbe wa barua pepe kutoka Mombasa, ujumbe ambao Rose aliweza kuukuta katika kompyuta ya baba yake alipojaribu neno la siri la kompyuta hiyo mala nyingi bila mafanikio. Alipojaribu tena na tena !,hasa baada ya kuandika jina Rose kwa herufi kubwa, kompyuta ya baba yake iliweza kufunguka na kumfanya Rose kupigwa na butwaa kwani hakutambua kuwa baba yake alikuwa katili kiasi kile. Aligundua mauaji mengi ambayo baba yake aliweza kuyafanya huku akijishugulisha na biashara haramu za magendo.



*****************



Raisi alitabasamu, huku akiwapongeza vijana wake kwa kazi nzito, kazi ya kugundua muuaji kupitia alama za vidole (finger prints) zilizoachwa katika bunduki ambayo muuaji aliitumia kumuua Jacob.



"Hii sura sio ngeni, lazima kuna sehemu tuliweza kukutana ",mheshimiwa raisi akiwa anaitazama sura ya muuaji katika kompyuta, aliongea huku akikuna kidevu chake, bila shaka alikuna kipele kwani hakubarikiwa kuota ndevu hata moja katika maisha yake.



"Mtu huyu akipatikana, lazima tutatambua siri nyingi nyuma ya pazia, haraka sana atafutwe! ",raisi aliongea na kutoa amli kwa vijana wake, huku akiondoka katika jengo la mamlaka ya mawasiliano Tanzania, TCRA …





Gari dogo aina ya Noah linapaki nje ya uwanja wa ndege wa mwalimu Nyerere ,ni baada ya safari ndefu yenye foleni ya magari mengi sana lakini hakuna chochote ambacho kiliweza kuhalibika.



"Ok goodbye mr Rodgers!, wahi ndege yaaani dakika kumi tu zimebaki ndege iweze kuondoka, foleni ya Morogoro road kidogo itucheleweshe kabsaaa! sunajua Mbezi mpaka hapa kwa mida hii ya jioni lazima jasho likutoke ……",mzee Jastin alimkabidhi begi kijana wake wa kazi, huku akilaumu foleni ya magari, foleni ambayo iliweza kuwachosha sana na ilikuwa imebaki kidogo tu waweze kukuta ndege imeondoka.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

"Sawa bosi, nikifika kisauni Mombasa ……nitakupigia simu, ngoja niwahi ndege ",ilikua ni sauti ya Rodgers, akipokea begi lake kutoka kwa bosi wake na kisha kuelekea sehemu ya abiria waliokuwa wakisafiri, tayali kwa ajili ya kuondoka haraka sana Dar es salaam.



********************





ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog