Search This Blog

Friday 18 November 2022

OKTOBA 15 RAIS ANAENDA KUFA - 2

 






Simulizi : Oktoba 15 Rais Anaenda Kufa
Sehemu Ya Pili (2)








Usiku huohuo aliamua kuondoka. Akiwa kajiweka vizuri kwa mapambano yatumiayo mkono na silaha ndogo za kimapigano ya karibu. Kisu! Ili lolote baya litalojiri aweze kukabiliana nalo. Mwendo ulikuwa wa kukimbia. Kwa kasi ya wastani, awahi kufika kabla mambo anayohitaji
kufanikisha hayajapeperuka. Baada ya mwendo wa dakika kadhaa, aliwasili nyumba husika. Hakusogea kwenye ukuta uliozunguka nyumba moja kwa moja, alitega kwanza sehemu, kuangaza mazingira yalivyo. Usalama wa eneo na vitu vingine pia. Alipojihakikishia pako shwari, alijisogeza langoni na kuanza kubisha hodi, kwa kugonga lango akiambatanisha na sauti ndogo. Alibisha takribani dakika tatu, pasi na kuwa na muitikio wa aina yoyote, hali iliyomshawishi ajaribu kusukuma aone kama kuna uwezekano wa kufunguka. Alisukuma, tena alisukuma kwa kadri ya nguvu alizohitaji kutumia. Kisha dalili fulani za mafanikio zilijitokeza zilizompa mwanga na uashirio kuwa lango halijafungwa. Kwa usiri na mnyato wa hali ya juu, alifanikiwa. Alifungua sehemu ndogo iliyomwezesha kuingia kisha kufunga.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Aliendelea kutembea kwa mnyato kulifuata jengo lilipo. Umbali mita sitini toka langoni. Lilikuwa jengo kubwa, lililokosa utofauti na kasri. Ama hekalu. Likipambwa na mandhari nadhifu, yaliyosheni maua na miti itengenezayo kivuli, jua liwakapo. Aliitumia miti kwa kificho, isiwe rahisi kuonekana, hadi alipolifikia kisha kuketi kiambazani. Mwanga hafifu wa taa zilizotegwa chini bustanini zilimuwezesha kuona mazingira ya jengo yalivyo, japo jengo husika lilitawaliwa na kiza, hakuna taa yoyote iliyowaka. Ijapokuwa zilikuwepo. Alivyojaribu kuchunguza madirisha usawa ule aliopo kutafuta ambalo liko wazi hakubahatika kuliona. Yote yalifungwa. Na yalikuwa madirisha ya vioo, hivyo alijiona mwenyewe. Ila hakukubali kirahisi. Kama lango lilikuwa wazi, basi na hapo kuna sehemu moja wapo lazima iwe wazi. Kuhakikisha hilo, alivaa glavus na kuanza kusukuma dirisha moja baada ya lingine, kuzunguka jengo zima. Aliyafikia karibu madirisha yote. Ila isivyo bahati hakuna ambalo lilikuwa wazi. Yote aliyopitia yalifungwa. Ni mlango wa kuingilia ndani, na dirisha dogo la choo lililo juu ukutani ndilo alisalia kulifikia. Wakati huo moyo wake ukiwa umejaa roho ya ushindwa, kutofanikiwa kumuona mhusika aliyemfuata, japo hakuwa na uhakika kama yupo. Vivyo hivyo alivyo, alizidi piga hatua na kuufikia mlango. Chap! Alishika kitasa akafungua, lakini aliambulia patupu. Mlango nao ulifungwa.

“Mmmmmmmh! Nimefeli,” alisema James kimoyomoyo, kauli iliyoambatana na uvuaji wa glavus alizovaa.



Baadaye alirudi nyuma kutathmini jengo lilivyojengwa. Hapo! Katika angaza yake ndipo alifanikiwa kuliona dirisha la choo, vioo vyake vikiwa vimevunjwa, na nondo kadhaa zimekunjwa. Ishara tosha, kuwa mahali hapo pamevunjwa. Alivyofanya tathmini ya kina, aligundua pia. Nyayo za buti, zilizoonyesha kupanda na kushuka, pasi na sahau nyuzinyuzi kwenye moja ya nondo zilizokatika. Alifanya tafakuri ya ghafla. Nini afanye. Aliyoipatia ufumbuzi dakika nane baadaye.

“Acha nipande. Nikajionee mazingra ya ndani yalivyo,” alisema James kimoyomoyo. Kisha kutafakari namna itayomuwezesha kuingia ndani kupitia hilo dirisha dogo, ambalo kwa mtazamo wa kawaida, asingeliweza ingia, sababu umbo lake ni kubwa. Ila alijipa moyo wa majaribio.



Alirudi nyuma hatua kadhaa. Takribani tatu, macho pima aliyatuma dirishani, na maeneo mengine, kuangalia kama anaweza fanikiwa kupata kitu kitachomuwezesha kupanda alifikie dirisha kisha aingie ndani. Baadaye ilimlazimu kuanza zunguka. Baada ya ile angaza yake kutoambulia chochote, mazingira ya karibu. Alizunguka huku na kule ndani ya uga huo, alitumia kama dakika nne, ndipo alifanikiwa kupata kitu alichoamini kinaweza kuwa msaada kwake. Mawe makubwa matatu! Aliyasomba, na kuyaweka chini usawa wa dirisha, aliyabebanisha. Alipojihakikishia yapo sawa, hayawezi mpatia madhara yoyote, alipanda juu ya mawe hayo. Na kukamata, zile nondo zilizokunjwa. Shughuli iliyofuatia, alijikokota kupitia miguu kuupanda ukuta. Mwili ulivyofikia dirisha, alitanguliza kuingiza kichwa ndani. Kazi ikasalia kwenye kiwiliwili. Kila alivyojaribu kung’ang’aniza kiingie, ilishindikana. Hadi ilifikia hatua kumpatia michubuko mabegani, mikono kukosa nguvu na miguu kushika ganzi, sababu ilikuwa inaning’inia hewani.



Harufu ya manukato ya sabuni, iliyopokelewa puani ilimlazimisha kuwa na nia ya kufanikisha kuingia. Asikate tamaa. Wazo lililokubaliwa akilini pasi na kipingamizi, ila mwili hukuridhia. Kwani, kila alivyoongeza jitihada za kuingia, ndivyo alijiongezea maumivu mwilini mwake. Mwishowe alichoka kabisa, kushuka ilimpasa. Alifanya hivyo, huku akiwa anahema kwa nguvu, dhihirisho la uchovu. Hali iliyomfanya ashuke taratibu, lakini ghafla! Sauti ya mlio wa risasi iliyopita pembeni yake ubavu wa kushoto, ulimharakisha kushuka pasipo mpangilio. Mshuko uliomuangusha chini vibaya mno. Aliangukia mgongo. Mwanguko huo ulianza mpatia maumivu ya uti wa mgongo, na sehemu ya mgongo kwa ujumla. Maumivu yakamjenga kuwa mateka kwa urahisi. Mbele ya mtu aliyepiga risasi, ambaye alishindwa mfahamu kutokana na umbali aliosimama mtu huyo. Ila umbo lilimpa picha, japo si ya uhakika, kuwa mtu yule ni wa jinsia ya kike. Katu, hakudiriki kufanya kitu chochote, zaidi ya kutulia tuli, atoe nafasi ya kumsogeza mtu huyo. Na kumpa nafasi nyingine pia, ya kutoshambuliwa.



Kama alivyohisi! Yule mtu, alikuwa ni mwanamke. Mama Tausi. Alijisogeza karibu na eneo alilolala James. Kujihakikishia matokeo aliyotaraji. Alisogea huku akiteta jambo, kumuendea James, aliyekuwa anataabika kugaagaa pale chini kuugulia maumivu kwa usiri, asionwe.

“Naamini u mzima. Maana sikuwa na lengo la kukuondoa ulimwenguni. Kabla sijakufikia, jitambulishe nipate kukufahamu,” alisema Mama Tausi, alipomfikia huku akiisundika bastola yake, aliyotumia kushambulia, kiunoni maeneo ya mgongoni.



Baadaye alimgeuza. Kisha kutumia kurunzi ndogo kummulika apate mfahamu. Bayana alimshuhudia. Miali ya mwanga ilivyotua barabara usoni mwake.

“Inuka. Tuelekee ndani,” alisema Mama Tausi, huku akimsaidia kuinuka pale chini.



Alivyoinuka waliongozana hadi ndani. Na kufikia sebulani. Moja kwa moja sofani, baada ya hapo Mama Tausi alianza toa huduma ya kwanza kwa James, katika majeraha yake yaliyoenea baadhi ya sehemu na mgongo pia. Shughuli hiyo ilivyohitimishwa walianza maongezi. Yaliyoanzishwa na James, kutokana na wingi wa shauku iliyokithiri moyoni mwake. Alianza kuhoji kuanzia mwanzo, siku ya kwanza waliyobahatika kuonana. Na nyingine zilizoendelea pasi na sahau mambo binafsi aliyonayo. Naye Mama Tausi kumjibu, alimpatia ushirikiano, pale alipoona kwa nafasi yake panafaa kushiriki.

“Namtafuta Joram Isaac. Unanisaidiaje kufanikisha hili?” aliuliza James.

“Unamfahamu?”

“Hapana.”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Na vipi kuhusu mmiliki wa J&I unamfahamu?”

“Nasikia sikia tu. Kuwa inamilikiwa na Mama naniii sijui…”

“Sina cha kukusaidia zaidi ya hivi viwili nitavyopata kukuelezea. Kwanza; aliyekupa hiyo kazi kakosea sana. Kwani, huu ni mchezo wa picha. Ili ufanikishe, lazima uwe na picha, ambayo ndiyo huwa mwanzo wa sakata. Maana hata nami niko ndani ya mchezo. Ila nafasi yangu ishaishia hapa. Mimi ndiye mtu pekee, niliyepaswa kukupatia mwangaza wa kazi yako. Huyo mtu aliyekutuma, alipaswa akutume kwangu moja kwa moja kabla hujaenda kwa wengine. Hao wanaopaswa kutafutwa. Mimi nitakukabidhi vitu viwili, vitavyokufanya ufunge kile kitabu nilichokukuta unasoma ile siku, na uipeleke akili yako katika hivyo vitu. James! Kazi uliyonayo ni ngumu. Omba mungu umalize salama, kwani ukikosea idara zima haitokutambua. Kama uonavyo hivi sasa. Wamekufungia mawasiliano kwao. Kurudishwa, ni pale utapomaliza kazi salama,” alisema Mama Tausi na kutulia kwa muda, takribani sekunde kumi kisha kuendelea.

“Nakupa hii picha, ukiidadavua, utaielewa na kuifahamu. Pasi na sahau na hii nyingine. Picha ya gari. Ukifanikiwa kuipata hii gari, utakuwa umefanikiwa kumpata mmiliki wa J&I. Kwani ndiye Joram Isaac unayemtafuta.”

“Mama!” aliita James kwa Mshangao.

“Ukweli ndiyo huo.”



James aliondoka, alipoona takwa lake lishakamilika, kurudi nyumbani kwake. Kule alikopanga. Akiwa na picha mbili za kuzifanyia kazi. Mosi; ilionyesha wazee wanne wakiwa wamesimama ubavuni mwa gari dogo, aina ya BMW. Picha ya pili nayo ilionesha gari dogo, hiyohiyo BMW ikiwa na namba za usajili zilizosomeka UG 05 MNG, nayo ikiwa na bango la taksi kwa juu. Kwa mtazamo tu wa awali, alitambua gari hiyo iliyoko kwenye picha zote ni moja, hivyo alikuwa na jukumu la kuitafuta ili apatiwe ufumbuzi. Nyuma ya picha, ni picha moja pekee, ilikuwa na ujumbe mwingine. Ile iliyojumuisha watu wanne. Ujumbe ambao ni tarehe, uliosomeka ‘08/07/1970’. Na kumfanya azidiwe na hamu ya kufanyia kazi muda huohuo.



Kweli! Punde tu, alivyowasili nyumbani kwake alianza utekelezaji wa jukumu. Hakutaka kulaza jukumu lake, lenye kila ishara ya kumwezesha mafanikio katika mpango mzima alionao. Alivuta kitabu cha kumbukumbu na kuanza kuperuzi, picha zilizo na taarifa ya tukio husika lililokwishafanyika miaka hiyo ya nyuma. Alipitia kurasa moja baada ya nyingine. Kitabu chenye kumbukumbu ya matukio ya muhimu yaliyotendeka tangu nchi yao ipate uhuru. 1962! Isivyo bahati, hakufanikiwa iona hiyo tarehe. Na alivyojaribu kuchunguza, aligundua karatasi moja wapo imechanwa. Ugunduzi uliomfanya, moja kwa moja ahisi, kuwa karatasi iliyochanwa ndiyo hiyo tarehe aliyonayo mkononi. Hakuwa na jinsi! Ilibidi atumie hisia, kutafakari, hadithi mbalimbali alizokwishazisikia hapo nyuma. Juu ya kufanya hivyo, hakuna mrejesho aliofanikiwa kupata, ulio na matumaini ya kumuonesha ile tarehe inahusiana na tukio gani. Baada ya kushindwa kuidadavua, alihamia pichani. Kuitafakari tukio lilikuwa vipi. Alitumia zaidi ya dakika ishirini na nne, huku akivuta taswira, picha kama hiyo ashawahi iona sehemu nyingine.

“Yes! Mapokezi ya Waziri Mkuu wa Uingereza,” alisema James kimoyomoyo. Na alivyotupa macho kwa umakini zaidi, alibaini uwepo wa watu wawili walioketi ndani ya gari. Wale waliosimama nje walionekana kulisindikiza gari hilo.



Alivyoendelea kuvuta kumbukumbu zaidi, akapata uhakika. Alichobashiri kipo sahihi. Picha hiyo ni ya kiongozi mkuu wa nchi ya Uingereza, ilipigwa siku aliyotembelea nchini Mangaka akitokea nchini Afrika Kusini, kwenye mkutano mkuu wa jumuiya ya madola. Watu waliosindikiza gari aliyopanda, pasi na kuwa na mihangaiko walionekana ni wamangaka. Asili ya ngozi yao iliwatambulisha. Tena walionekana kuwa walinzi, waaminifu waliopendekezwa kumlinda kiongozi huyo, akishirikiana na walinzi aliokuja nao. Sasa alihamia kwa hao watu, mmoja baada ya mwingine. Ila ilimuwia ugumu fulani, uliomshinikiza kusitisha kwa muda na kuhamia kwenye magari. Sababu sura za wale walinzi wasindikizaji zilikosa ufanisi wa kuonekana vizuri. Sura zao zilijaa ukungu. Aliiacha ile picha chini, kisha kuivuta nyingine aliyonayo. Aliitathmini kwa kina, na kuioanisha na ile iliyombeba Waziri Mkuu wa Uingereza. Zilifanana. Ila ni namba tu ndizo zilitofautiana. Namba za usajili. Ile iliyombeba Waziri Mkuu, ilikuwa na namba ya taifa la Uingereza. Iliwekwa kwa shughuli hiyo maalumu. Ila namba yake halisi, ni ileile iliyoko kwenye picha nyingine.



Tathmini hiyo ilimfanya akumbuke jambo. Alimkumbuka Mashaka. Dereva taksi pekee anayemiliki BMW kufanyia shughuli hiyo. Alienda mbali kwa kukumbuka maongezi yao pia, jioni moja James alivyohitimisha biashara yake. Alitumia muda mwingi kumhoji Mashaka kuhusu historia ya maisha yake. Hakuishia hapo. Aliendelea na kumbukumbu, ya kukumbuka nyaraka mbalimbali za gari analomiliki Mashaka. Hapa! Ilimfanya apate mhemo, wa nguvu ulioashiria kujidharau.

“Mashaka! Unanifanya mjinga?” alijiuliza James, baada ya kupata uthibitisho wa hisia zake.

“Mashaka! Kumbe wewe ndiye Joram Isaac? Ninayehangaika usiku kucha kukutafuta?” aliendelea kujiuliza. Taratibu nguvu zikimuishia. Alikosa morali ya kuendelea kufanya kazi. Mwishowe alipitiwa na usingizi.



Alivyozinduka, alianza mfikiria upya Mashaka. Kwamba ni kijana wa aina gani? Na kwanini alikuwa kajificha. Alitumia zaidi ya nusu saa, kufanya tafakuri yake, pasipo kupata muafaka, hatimaye kufikia maamuzi ya kumtafuta siku iliyofuata. Siku ilivyowadia, mapema sana. Saa 12 asubuhi, aliwahi kituo cha taksi, kilichopo eneo lile alilofungua kituo cha huduma ya kusafisha viatu. Ambapo Mashaka naye alikuwa anatolea huduma yake. Alikuta baadhi ya madereva washawahi, ila Mashaka bado hakuwasili. Hivyo aliwauliza aliowakuta, nao kumjibu walivyohisi.

“Labda kamwangalie nyumbani kwake. Halafu mbona ulikuwa umeadimika sana kwa hizi siku za kati?”

“Acha kaka, ni maisha tu. Tutahabarishana juu ya hilo jambo baadaye, acha nimuwahi kwanza Mashaka nyumbani kwake kabla hajaondoka,” alisema James, wajihi ukimuonesha kuwa na mambo mengi yamtatizayo.

“Hee! Uko wanguwangu sana ndugu yangu.”

“Tutajuzana kaka usiwe na papara.”



Himahima alikaza miguu, kuitafuta nyumba ya Mashaka ilipo. Ambaye ndiye Joram Isaac. Lakini inawezakanaje kuwa yeye? Maana ana umbo dogo, mwembamba, hivyo muonekano wake ulimfanya kuwa kijana. Kwani hata wajihi, hukuwa hata na chembe ya kunyanzi. Ila kijana aliweza vipi kuhusika katika shughuli za ukombozi? Ulikuwa mtihani mwingine, kwa James, uliomhitaji akili ya ziada kupata jibu lililo sahihi. Uwiano ulikosekana. Na ili aoanishe ilimlazimu akutane naye amueleweshe. Mwendo wa dakika kadhaa baadaye alifanikiwa kuwasili nyumbani kwake, alibisha hodi, bila mafanikio. Haikuitikiwa! Lakini kwa mbali alisikia sauti ikiugulia maumivu, toka ndani ya nyumba hiyo. Alivyojaribu kusukuma mlango, ulifunguka. Aliangaza huku na kule, alivyoona hakuna mtu, aliingia ndani na kumkuta Mashaka kalala chini, hoi bin taaban, akitapatapa huku na kule kuugulia, damu nyingi ikiwa imetapakaa sakafuni, mkononi kakamatia picha na kuna kitu kingine kilikuwa pembeni yake ambacho James hakuweza kukitambua kwa urahisi. Chap! Alipiga goti chini kumsogelea. Apate kufahamu undani uliopo hata kama alionekana kuwa na dalili tosha za kutoendelea kuwepo ulimwenguni. Ila kilichomshangaza, sura aliyokutana nayo, ilikuwa ni sura tofauti na ile ya siku zote, aliyozoea kuiona. Leo ilionekana sura nyingine kabisa. Sura iliyo na kunyanzi kwa kiasi fulani. Sura ya kizee!

“Ina maana alikuwa anatumia sura bandia?” aliwaza James, wakati huo akivichukua vile vitu alivyokamatia Mashaka.

“James!” Mashaka aliita. Kwa sauti ya tabu sana, iliyosikika kwa mbali. Hali iliyomfanya James ashangae, kwani siku zote alijitambulisha kwa jina la Sadiki. Na Mashaka, ambaye ndiye Joram Isaac alitumia jina hilo kumuita.



James! Alishangaa. Kafahamika vipi ilhali alikuwa hatumii hilo jina. Mshangao ulioonekana kwa Joram pia.

“Usishangae, mimi nakufahamu toka muda. Japokuwa ulidiriki kutuongopea pale kijiweni, ila nikaona si tatizo. Awali naomba unisamehe, kwa nami kukuongopea pia, nilifanya hivyo kwa usalama wangu. Kwani ningebainika mapema, ningefanyiwa hiki nilichofanyiwa. Na usingeliweza kupata dondoo za kazi uliyoagizwa. Japo tayari nishabainika,” alisema na kutulia kwa muda kisha aliendelea…http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“James, mimi ndiye mtafutwa. Uliyekuwa unahangaika siku zote kunitafuta. Naitwa Joram Isaac na si Mashaka kama ulivyokuwa unanifahamu. Naamini leo ni siku yangu ya mwisho duniani. Ila sitaki kuondoka pasipo kukupatia ujumbe wenye msaada mkubwa kwako na Rais pia.”

“Twende nikuwahishe hospitali,” alisema James huku akijaribu kumuinua.

“Hapana! Tushachelewa. Pia nikienda huko, watakuja tu kunimaliza. Maana hawa watu lengo ni kutuondoa ulimwenguni. Mimi na timu yangu kwa ujumla. Ndani ya hiyo timu, Rais yuuu...” alisema Joram, ila hakuweza malizia kaulia yake, kutokana na hali kubadilika ghafla na kuzidi kuwa mbaya.

“Joram! Joram!...niambie ulichonacho,” alisema James huku akimtingisha.

“James! Oktoba!...oktoba!...”

“Imefanyaje?”

“James! Oooooo...oktoba 15,...Rais!...Rais…aaaaaaaa...anakwenda kufa,” alisema Joram. Mkono mmoja akiwa kanyoosha juu na kutulia. Ishara kuwa kashaaga dunia.



James, alijaribu kumtingisha huku na kule akimuita jina lake, ila hamna kilichoendelea toka kwake. Tayari alishaondoka duniani. Aliishia kumtazama, baadaye alikitathmini kile kitu ambacho mwanzo hakukielewa na kukuta kuwa ni sura. Ile aliyokuwa anaifahamu. Hivyo kufanya kile alichohisi mwanzo kuwa sahihi. Joram alikuwa anatumia sura bandia. Kwa heshima. Aliufunika vyema mwili wake kisha aliondoka. Aliondoka, akiwa na mawazo mengi sana. Hadi alivyowasili nyumbani kwake, kichwa hakikuacha muuma. Alivyofika, alifikia mapumziko mafupi. Kupumzisha akili kwa muda fulani, alivyoamka, aliinakili ile kauli kwenye kitabu chake cha kumbukumbu, kisha kuanza kutafakari, kina nani wamesababisha mauaji yake. Na nani anaenda kumuua Rais hiyo siku aliyotajiwa. Siku ya kusherehekea taifa lao kupata uhuru.







Alienda mbali zaidi, kutathmini mazingira yatavyokuwa, na taswira ya mauaji ya aina gani yatatumika. Kwa namna ulinzi unavyokuwa mkubwa, mkali na ujazo wa watu.

“Wadunguaji. Ndiyo watatumika,” alijisemeza baada ya kuvuta picha kwa muda mrefu.

“Inabidi niwapatie taarifa hii uongozi wangu. Lakini nitawapatia vipi, ilhali mawasiliano nao nishafungiwa?” aliendelea kujisemea. Mwishowe alipitiwa na usingizi kwa mara nyingine.

****



Sauti za watu wengi walioonekana kuisogelea nyumba yake ndizo zilimuamsha. Maana zilikuwa sauti za juu, zenye mabishano huku wakizidi kusonga mbele.

“Haina haja ya kumpeleka kituo cha polisi. Tunapiga kama alivyompiga na kumuondolea uhai mwanetu. Kijana wa busara.”

“Sahihi. Tulimuona kuwa mkarimu kumbe ile ni ngozi tu? Roho yake haiko hivyo. Imejaa ukatili, na dhuluma. Basi leo ataonja joto la jiwe.”

Ni kauli zilizosikika toka kwenye halaiki hiyo, iliyojumuisha zaidi ya watu hamsini, wa kila jinsia na rika tofautitofauti, ila asilimia kuwa walikuwa wenye umri uliozidi miaka kumi na nane. Na kusikika vyema masikioni mwa James. Nitajitetea vipi? Ndilo swali la kwanza alilojiuliza, ili aokokane na hatari iliyomnyemlea.

“Hawawezi nielewa hata nikijieleza namna gani. Mbadala ni kuondoka tu,” alijisemeza wakati huo akitafakari sehemu ipi atumie kuwakimbia pasipo onekana.



Nje! Wale watu walianza izunguka nyumba na baadhi yao kubisha hodi. Tena kwa nguvu mhusika asikie vyema. Kwani mazingira waliyokuta mlangoni yaliwapa utambuzi kuwa kuna mtu ndani. Mlango ulikuwa umefungwa kwa ndani. Walitumia muda mrefu pasi na mafanikio, hali iliyowashawishi kuchukua maamuzi mengine ambayo awali hawakuyapangilia.

“Kama vipi tuchome tu hii nyumba. Haina kujalisha kapanga ama ni yake.”

“Yeah! Huo ndiyo mbadala na fundisho kwa wengine wenye nyumba wanaopangisha wageni. Ili wapate kukoma mara moja tabia hiyo kuiacha.”



Lolote lililotamkwa, lilipita pasipo jadiliwa. Hivyo haraka sana watu kadhaa walijitoa kufuata mafuta ya petroli na kurudi dakika chache baadaye. Hawakupoa! Punde tu mafuta yalivyowasilishwa, yalimiminiwa kwenye paa. Ambayo ilikuwa ya nyasi kisha njiti zilizowashwa zikatupwa juu yake. Naam! Moto ulifana. Nyasi uliupokea vyema na kuruhusu uteketezi, taratibu kumaliza jengo zima ambalo James alipanga. Tena kwa hasira kali walizonazo, hawakuhitaji kitu cha aina yoyote kitoke ndani kwa kile walichofanya, hivyo walitafuta kufuli wakafunga mlango, kisha walisogea pembeni kusikilizia kinachoendelea. Shangwe na nderemo zilianza enea. Toka kwa wale wachomaji kufurahia kinachoendelea. Walipiga nyimbo. Ya kila aina pasi na sahau mbizi. Taratibu walijikusanya pamoja. Kwani, baada ya kuchoma na kutosikia vurugu zozote toka ndani waliamini hamna mtu. Ndipo walitoka kwenye hizo kona walizosimama walizokuwa wanadumisha ulinzi.



Wakati wote James alikuwepo ndani. Akili ikipambanua mbinu ipi aitumie kujiokoa. Maana hali ilikuwa tete, na alilazimika kuwa salama, ili kile alichoagizwa kikamilike. Alipambanua kwa dakika kadhaa, alipopata muafaka wa kipi afanye, alianza kutekeleza. Kubomoa sehemu ya ukuta wa jengo. Dirishani! Harakaharaka alianza fanya kazi hiyo. Kwa nguvu kiasi wale watu wa nje wasisikie. Kilichomsaidia, nyumba ilikuwa imejengwa kwa tope. Nyumba ya miti, hivyo ukuta wake ulikuwa mwepesi kubomoka, ila kasi na ongezeko la moto, lilimuathiri. Kwani joto lilizidi ongezeka, pasi na sahau moshi. Nao uliongezeka, na kutanda nyumba nzima, hali iliyopelekea kumzuia James asione mbele. Vilevile kumpunguzia nguvu na kasi ya upumuaji, hatimaye alianza ona mawenge, kifua kikambana, mwishowe alidondoka na kupoteza fahamu.



Moto ulizidi shika kasi, na kuunguza baadhi ya vitu vilivyopo chini, achilia mbali paa. Hali iliyopelekea kuendelea kuwafurahisha wachomaji, kwa kuimba nyimbo mbalimbali zenye morali. Huku wakichezacheza kwa aina tofauti za mitindo. Kila mmoja na mtindo wake. Baadaye ulimfikia James pale chini. Ulianza kumuunguza, taratibu, kwa kuanza mavazi aliyovaa kisha kufuatia ngozi yake. Wakati huo wote, bado alikuwa hajitambui. Hata chembe ya dalili za kuzinduka hazikuonekana. Kana kwamba tayari alikwishapoteza maisha.



Dumu lililo na maji, na kufungwa katika moja ya mti, ama nguzo zilizoshikilia miti mingine, lilivyoungua na kuruhusu udondokaji na umwagaji wa maji yenye jotojoto kiasi, ndilo lilimzindua baada ya kumdondokea. Alivyozinduka, alijaa mshangao, hajui nini afanye ukizingatia moshi ulizidi kuwa mwingi na moto ulioshika mwilini mwake ulizidi muunguza. Alijaribu kujipigapiga ili auzime, lakini wapi, hukuzimika. Na nguvu ya kupumua ilianza upya kumuishia, ishara nyingine anaenda kuzima. Hakuwa na budi, alilazimika kupiga kelele kuomba msaada ayanusuru maisha yake. Kwani vinginevyo, anaenda kuaga dunia. Kwa sababu alikuwa karibu na ukuta, alivyokuwa anapiga yowe la kuomba msaada, aliambatanisha na kitendo cha kupiga ukutani. Alipiga yowe sana, lakini si kwa muda mrefu, kwani moshi ulimuingia kooni na kubana kifua.



Naam! Sauti aliyoitoa ilisikika, kwa baadhi ya watu walioko nje. Wale waliochoma, na watu wa idara za ulinzi na uokoaji, ambao waliwasili mahali hapo, dakika kadhaa baadaye walivyofikiwa na taarifa. Haraka sana, wote walijazana, upande ule sauti ilikosikika. Waokoaji, toka jeshi la zimamoto na uokoaji walio na mavazi rasmi ya kujikinga na moto, wakisaidizana, na askari wa jeshi la polisi, walibomoa ukuta kisha kuingia ndani. Huku wakiwa na tochi kubwa, zitoazo miali mikali ya mwanga ili ziwasaidie kuona. Waokoaji walivyoingia, nje, askari polisi, kazi yao kubwa ilikuwa kutawanya wale watu wasikaribie na wengine walioleta ubishi waliwakamata na kuwapeleka kituoni. Pia kutengeneza mazingira rafiki ya uchunguzi pindi moto utapomalizika. Isivyo bahati, sehemu waliyobomoa haikuwa sahihi. Pale sauti ilipotokea. Hivyo iliwabidi wazunguke huku na kule, na baada ya dakika kadhaa, walifanikiwa kuuona mwili, ukiwa umelala chini, huku sehemu kubwa ukiwa umeungua na unaendelea kuungua. Pasi na chelea, waliutwaa juujuu kisha kutoka nao nje. Na kupokelewa na yowe kubwa la wananchi walioshinikiza mtu huyo auwawe.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Walionyesha shinikizo lao kwa kutupa mawe, fimbo na zana mbalimbali japo polisi walijitahidi kuwazuia. Kwa kuwatawanya waondoke eneo hilo, lakini ilishindikana, hadi ilifikia hatua ya kutumia nguvu kadri kuhakikiksha watu hao wanaondoka. Moja kwa moja mwili wa James ulipelekwa ndani ya gari. Gari ya wagonjwa, ukiwa tayari ushazimwa moto kisha safari ya kumpeleka hospitali ikaanza. Mwendo wa dakika tisa, gari ilifanikiwa kuegeshwa karibu na korido litumikalo kuteremshia wagonjwa, ama miili ya wafu, waliotolewa ajalini na sehemu zingine itakiwapo kuhifadhiwa chumba maalumu cha miili hiyo. Monchwari! Katika hospitali ya mji wa Lukwika, iliyopo mtaa wa Cheleweni. Aliteremshwa kwa haraka, punde alivyobainika kuwa bado ni mzima, kisha akakimbizwa chumba cha daktari. Himahima akapokelewa, na madakatri wawili wa kike, walioiva mvi nyingi kichwani. Na kunyanzi katika ngozi zao, ishara tosha kuwa wana umri mkubwa. Miaka yao zaidi ya sitini. Walikwishastaafu, ila walirejeshwa kazini, baada ya upungufu wa madaktari nchini katika kitengo walichopo. Madaktari bingwa wa ngozi. Hawakuwa pekee, walikuwa sambamba na manesi wawili, waliokuwa wanahangaika huku na kule, kuandaa mazingira wezeshi kwa ajili ya mgonjwa.

“Apelekwe ICU,” aliamuru mmoja baina ya madaktari wale, alivyoona hali ya James kuwa ni mbaya, na haifai kupatiwa huduma ndani ya chumba hicho.



Dakika saba baadaye, tayari James alikuwa juu ya kitanda, ndani ya chumba cha wagonjwa mahututi. Madaktari, wakiwa wameongezeka, toka wawili hadi sita, na wauguzi wanne, waliokesha muda wote kuzunguka kila upande wa chumba hicho. Jopo hilo lilikuwa chini ya Dkt. Kanyunya, ambaye ni mganga mkuu nchini Mangaka, anayefanya kazi hospitali ya taifa iliyopo mjini Lidede. Alisafiri kwa uharaka, kwenda kushughulikia tatizo hilo baada ya kupatiwa taarifa toka wizarani, Wizara ya afya. Ili akasaidie kuyanusuru maisha ya mtu huyo, pia kwenda kuficha na kuzuia aibu inayoikumba mara kwa mara hospitali ya mji huo ya uzembe unaopelekea kupoteza wagonjwa wengi wakiwa wanapatiwa matibabu. Dkt. Kanyunya, mwanamama hodari, shupavu na bingwa wa magonjwa ya moyo, akisaidizana na wale wengine aliowakuta, mabingwa wa ngozi, hivyo kufanya madaktari bingwa kuwa watatu, walishirikiana kwa hali ya juu, pasi na yeyote kumdharau mwenziye ili wakamilishe salama salimini jukumu lililopo mbele yao. Na kuondoa aibu na kashfa pia, iikumbayo hospitali hiyo.



Ilikuwa kazi ngumu, iliyochangia kwa kiasi kikubwa, jasho kuwatiririka muda wote, ijapokuwa chumba kilitawaliwa na ubaridi wa wastani. Ulioenezwa na kiyoyozi, na hali ya hewa iliyopo, katika mazingira hayo ya hospitalini. Leso zao zilifanya kazi ya ziada kulikausha, ili lisipate dondekea mwilini mwa mgonjwa na kuleta madhara mengine. Pale hali ilipozidi, mmoja wa manesi hakusita kufanya kazi hiyo, kwa kutumia taulo maalumu la kila daktari anayehudumia, kuwafuta. Kutokana na hali aliyonayo, alifanyiwa upasuaji wa baadhi ya maeneo, kisha kuchukua sehemu ya nyama iliyopasuliwa kuziba sehemu nyingine, hasa mdomoni. Ili uwe katika umbo lake la kawaida. Pia aliunganishwa na mashine mbalimbali. Za kupumulia, za kupandisha mapigo ya moyo na nyinginezo. Pasipo sahau dripu za maji na damu, zilibadilishwa kila baada ya dakika chache, kwa sababu zilikuwa na uhitaji mkubwa na zilitumika kwa wingi.



Sehemu zisizo na madhara makubwa, zile zilizoungua, alipakwa dawa, kisha kufungwa bandeji ngumu kidonda kisiharibike. James, alipatikana. Kwani mwili wake haukutamanika, uliungua vibaya mno, na kutengeneza rojojo, hasa sehemu zenye mafuta mengi. Achilia mbali weusi, uliopoteza uhalisia wa rangi yake kabisa. Jinsi alivyo, laiti mtu yeyote angeliukuta mwili wake barabarani, pasi na usumbufu, moja kwa moja angelitambua kuwa tayari, ashaondoka duniani. Hakika hakutamanika! Mwili wake ulileta kinyaa na uogofyaji kwa baadhi ya watu. Wale walio na imani ndogo, hawakuacha kuweweseka, kila muda wakumbukapo tukio hilo.







Kwa jitihada za madaktari, saa tisa baadaye, tayari walikwisha kamilisha kila kitu. Matibabu yalikamilika, na kuondoka chumbani, nyuso zikionyesha uchovu wa hali ya juu. Kwa sababu hawakupata chakula kwa muda wote waliofanya kazi. Baadaye taarifa za tukio hili zilianza enea. Kupitia tetesi za hapa na pale zilizokuwa zinaenezwa na wananchi. Mpaka zikawafikia polisi. Kwamba yule aliyepelekwa hospitalini kahusika na Mauaji ya Joram Isaac, ambaye wao walimfahamu kama Mashaka. Tetesi hizo ziliwafikia polisi, na kuwahimiza kuzifanyia kazi, kwa uharaka. Ili waweze kuthibitisha kama ina usahihi ama haina ndani yake. Hivyo Mkuu wa kituo cha polisi (OCS) ndani ya mji huo wa Lukwika, akisaidizana na timu ya upelelezi ya wilaya, walituma vijana wao kadhaa, kwenda kuthibitisha hilo. Wapatao vijana wanne, wenye taaluma mbalimbali za ulinzi na usalama. Vijana hao walijigawa. Wawili hospitalini, wengine, nyumbani kwa Mashaka, kwenda kuuchunguza mwili walioelezwa. Hawa waliongozana na raia kadhaa, waliowatumia kwenda kuwaonyesha nyumba husika.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Hawakutumia muda mrefu kuwasili. Kwani walikuwa wametumia usafiri wa gari kuelekea huko. Walivyoteremka garini, walianza chunguza mazingira ya nje ya nyumba yalivyo. Huku wakipiga picha baadhi ya vitu, walivyoamini vinaweza wasaidia katika kazi yao baadaye. Kwa kutumia simu za kisasa, na kamera za kisasa pia, zilizojaliwa ubora. Baada ya hapo waliingia ndani, walipokelewa na kiza kikali, kilichowalazimisha kuwasha tochi zilizopo kwenye simu zao waweze kuona. Mazingira tu, yaliwapa utambuzi, kwamba, hapo kuna kitu kibaya kimetendeka. Kwani damu nyingi ilikuwa imetapakaa chini, vyombo na vitu mbalimbali vya samani vilikuwa shaghala baghala, walivyoifuatilia ilikoelekea, waliambulia kukutana na dimbwi kubwa, na si vile walivyotaraji. Napo walipiga picha na kuchukua baadhi ya vitu, kama ushahidi kwa siku za baadaye. Kwa uhitaji wa kujiridhisha zaidi. Walizunguka vyumba vyote vilivyopo ndani ya nyumba hiyo na sehemu nyinginezo za ndani. Lakini hawakuuona mwili wa mtu ama kitu chochote. Hatimaye walirejea nje, jasho jingi likiwa linawatiririka, kwani ndani walimoingia mlikuwa na kiwango kikubwa cha joto.



Nje! Nako walijaribu izunguka nyumba yote. Na maeneo jirani yanayozunguka, lakini hakuna lolote walilofanikiwa kuliona. Baadaye walipiga simu kwa afande wao. Mkuu wa kituo, Mrakibu Msaidizi (ASP) Nendakulola Geugeu. Kamanda anayeaminiwa na jeshi la polisi katika majukumu mbalimbali ya kioparesheni za ndani. Ni aalimu, wa masuala ya matumizi ya mbinu mbalimbali za kimapambano. Pia ni mtaalamu wa sheria, na mbobezi wa upelelezi.

“Afande! Kweli, tukio limetendeka, ila mwili wa mhusika haupo. Hivyo haifahamiki kama ni mzima, ama tayari ashafariki kama tulivyoarifiwa. Na tumejaribu kuzunguka kila kona ya jengo, ndani na nje hamna chochote,” alisema mmoja baina ya wale askari kwa kutumia Radio maalumu, zitumiazo mawimbi kuwezesha mawasiliano.

“Siafu! Siafu, hongereni kwa kazi. Hakika yangu, mmetekeleza jukumu ipasavyo. Hivyo nguvu ya mwanga, kasrini,” alisema Asp Nendakulola. Kauli aliyoitoa ikiwa na mchanganyiko na maneno maalumu ya kiusalama, yaliyojaa kificho, yatumikayo ndani ya jeshi la polisi katika mji wao watu wengine wasifahamu nini kizungumziwacho.

“Nguvu moja! Uelekeo kwako,” alisema mmoja wa askari wale, huku wakipanda garini na kuondoka.



Upande wa askari walioelekea hospitalini, mambo hayakuwa mabaya. Walivyowasili na kujitambulisha, kwa Mganga Mkuu wa hospitali hiyo, na kueleza nia yao, waliongozwa moja kwa moja hadi, chumba cha wagonjwa mahututi watekeleze kilichowapeleka kisha waendelee na majukumu mengine. Walivikwa mavazi maalumu, ndipo waliongozwa kuingia chumbani. Walivyoingia, hawakukawiza. Mapema tu, walianza fanya kile kilichowapeleka. Ambapo walipiga picha za mnato pamoja na video, baada ya hapo walirejea kituoni. Walivyorudi, walifikia kwenye kikao cha dharura. Kilichoongozwa na Kamanda wa polisi mkoa wa Michiga, Kamishna msaidizi wa jeshi la polisi (ACP) Eng. Loloo Bwire. Kilikuwa kikao kifupi, kilichohusu, kubainisha ushahidi uliopatikana kabla haujapelekwa chumba maalumu cha kumbukumbu, kitumikacho kutunza vyanzo mbalimbali vya ushahidi.



Vyote vilivyopatikana vilimwagwa mezani, picha za mnato zilizopigwa, zilisafishwa na kujumuishwa hapo pia. Pasi na sahau, picha za video, ziliunganishwa kwenye skrini kubwa waweze kujionea vizuri kilichopo. Mikononi wakiwa wamevaa glavus, ili wasipate acha alama ya vidole vyao, kwenye vyanzo hivyo, walichambua kimoja baada ya kingine, walipoona kina watatanisha, walikijadili kwa muda, walivyofikia muafaka, waliendelea na kingine. Walifanya hivyo, hadi walivyoifikia picha ya mnato, inayoonyesha sehemu ndogo ya sura ya James, kwani kuna upande mwingine, karibu na jicho lake uliungua, sambamba kabisa na sehemu ya mdomo. Hivyo kufanya uso wake, upoteze muonekano uliozoeleka. Ila, hawakujalisha hilo. Waliichunguza vivyo hivyo, kwa umakini wa hali ya juu, huku wakivutia hisia, sura halisi ni ipi. Zoezi hilo liliwachukua zaidi ya dakika arobaini na tano, hadi kufikia muafaka na kuweza kufahamu. Baada ya kuhisihisi.

“Tafuta picha ya Rais Mlunji aliyoambatana na mlinzi wake,” alisema Kamanda Eng. Bwire, baada ya kufikiria kwa muda mrefu, kufananisha.



Mmoja wao alivuta kompyuta mpakato, kusogeza karibu yake. Aliiwasha kisha kuanza kutekeleza kile alichoamriwa. Aliingia mtandaoni, aliandika jina la Rais, baada ya hapo orodha ya picha nyingi zilitiririka. Alizifuatilia, kwa kushuka chini. Alivyoiona picha iliyomuonesha mlinzi wa karibu wa Rais Mlunji sawia, aliipakua, ilivyofika ujazo wa asilimia mia moja, alikata na kuelekea kwenye faili lililohifadhi ile picha. Akafungua! Ilichukua sekunde chache kufunguka, baada ya hapo, picha hiyo ya mnato ikajibainisha, na kutoa fursa kwa wote kuiona vyema.

“Afande! Ndiye mwenyewe.” Walijikuta wameropoka wote kwa pamoja.



Chap! Ilifananishwa na ile nyingine iliyopigwa hospitalini. Walivyoona imejaa ufanano wa kila kitu ijapokuwa ile ya hospitalini imesheheni dosari walifunga mada. Na kuwafanya waingie kwenye tafakuri ya kina kuhusu tukio lililojiri. Walijadili kinaga ubagha, baada ya hapo Kamanda Eng. Bwire, alivuta mkonga wa simu yake ya mezani. Alibonyeza vitufe kadhaa, kisha akaweka sikioni. Alisikilizia kwa sekunde chache, ilipopokelewa, akaanza maongezi na mtu wa upande wa pili. Kutokana na ukubwa wa sauti, iliwawezeaha hata wale wengine wasikie kinachozungumziwa.

“Ndiyo kiongozi!” alisema Kamanda Eng. Bwire, punde simu ilivyopokelewa.

“Endelea kiongozi,”alisikika yule mtu wa upande wa pili wa simu. Ambaye ni Mkurugenzi wa usalama wa Taifa, Knl. Mstaafu Faidha Mwembere.

“Kamanda wa polisi mkoa wa Michiga. Nina moja la kushangaza.”

“Lipi tena?”

“Una taarifa zozote kuhusu mtu wa karibu wa kiongozi wa nchi yetu?”

“Aaaah! Hayupo nchini kwa sasa. Kulikoni?”

“Hayupo nchini?”

“Ndiyo!”

“Kuna mtu yupo mikononi mwetu anatuhumiwa kufanya mauaji. Ila afya yake si nzuri. Tulivyomtathmini kwa kina tumetambua kuwa ni yeye. Mlinzi wa karibu wa Rais. Sasa unavyoniambia hayupo nchini, unanishangaza.”

“Ukweli ni huo. Duniani wawili wawili. Hivyo yumkini huyo kafanana naye tu.”

“Huwezi tuma mtu ili aje kuhakikisha?”

“Aaaah! Kuhusu hilo, nipe muda. Baada ya siku tatu nitakupa mrejesho.”

“Sawa.”



Simu ikakatwa.



Mshangao ndiyo kitu cha kwanza walichokionyesha, punde maongezi yalivyomalizika. Tena wote, na si mmoja. Inawezekanaje? Ilhali washamtathmini vya kutosha na kujiridhisha kuwa ndiye mwenyewe.

“Ila najua sababu, kwanini wamefanya hivyo,” alisema Kamanda Eng. Bwire.

“Ipi hiyo afande?”

“Kwa ajili ya kulinda idara yao, ili isionekane inahusika na matukio ya kiuhalifu nchini.”

“Mmmmh!”

“Hawa wako tofauti na idara zingine. Wanakanana waziwazi.”

“ Wanashughuli pevu.”

“Tena vibaya mno.”



Kikao kilihitimishwa, kwa kuweka mikakati kabambe ya kukabiliana na jambo hilo. Kwanza; kuhusu kupotea kwa mwili wa mtu waliyearifiwa, pili; juu ya mtu huyo, waliye na uhakika nayo kuwa ni usalama wa Taifa, na mlinzi wa karibu wa Rais. Mwili unapotezwa vipi? Ndicho kikubwa. Kilichowafikirisha na kuwatatanisha sana. Pindi wao, wanatafuta mbinu za utatuzi, mtaani nako, mambo yalizidi haribika. Wananchi walijawa tetesi kuhusu James. Zilizowashinikiza kutafuta habari kwa kina, walivyozithibitisha walianzisha vurumai, kuwahimiza polisi wamchukulie hatua. Walitanda barabarani, na kuzunguka taasisi mbalimbali za serikali, wakiwa na bango zilizoelezea hisia zao juu ya mauaji yaliyotendeka. Ijapokuwa, jeshi la polisi lilijidhatiti katika kuhakikisha hali inakuwa sawa, wananchi wanaoandamana wanasitisha mara moja, mpango huo, lakini hali haikutulia. Wananchi walikuwa wabishi, na waligoma usitishaji. Hivyo kuwafanya polisi, wazidishe nguvu ya upambanaji dhidi yao.



Chafuko lilifana, kila kona ya mji wa Lukwika, wananchi walipamba moto kushinikiza James (Sadiki) achukuliwe hatua atapobahatika kupona, polisi nao, walipamba kuhakikisha wanazuia, ili yasitokee madhara mengi. Hata wananchi wa miji mingine, walivyofikiwa na taarifa, kuhusu chanzo cha kile kinachoendelea ndani ya mji huo, waliunga mkono. Kwamba kile kifanywacho na wananchi ni sahihi, kwa kuwa watu wa idara hiyo hulindwa sana, wabainikapo wamefanya tukio la uhalifu. Hali ilivyozidi, na askari walivyobainika kuzidiwa, waliomba nguvu ya askari toka miji mingine. Kitendo hicho kiliibua wananchi wa miji mingine pia, kuanzisha vurumai kusaidia wale wa Lukwika.



http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Wakati wote, James alikuwa hospitalini. Fahamu yake ikiwa bado haijarejea, ila dalili za uzima ziliendelea kuonekana. Huduma nazo za matibabu aliendelea kupatiwa, tena akiwa chini ya ulinzi mkali wa askari polisi, walioagizwa kuhakikisha hadhuriki, na pale atapopata nafuu, kama sio kupona kabisa, afikishwe kituoni. Hatihati ya vurumai lililoanza kuwa kubwa zaidi ilionekana. Kwani, wananchi walitanda kwa wingi maeneo ya karibu ya hospitalini na kituo kikuu cha polisi cha mji wa Lukwika. Wale waliotoka miji mingine nao, baadhi walijumuika Lukwika, wengine, Makao Makuu ya jeshi la polisi, mjini Lidede. Kusisitiza haki itendeke katika hilo. Juu ya mara kwa mara, kufanyika upatanishi, toka kwa viongozi mbalimbali wakuu wa majeshi, na taasisi zingine za kutetea haki za binadamu na zile za kisheria, lakini hakukuwa na muafaka. Wananchi hawakuamini, kile waambiwacho. Kwa madai, vyombo hivyo vimezoea kutoa kauli zisizotekelezeka.

“Tunahitaji kumuona huyo mtu akiitwa jina lingine, si hilo lifahamikalo. Na kama serikali yetu haijawahi kunyonga mtu aliyehukumiwa kunyongwa basi, yapasa huyo kuwa mtu wa kwanza. Apandishwe kizimbani, hukumu yake, anyongwe. Na anyongwe kweli. Maana hao watu wamezoea kuonea raia wasio na hatia, kwa maslahi ya kulinda watu wengine wenye nguvu,” walisikika baadhi ya wananchi, katikati ya halaiki. Kauli waliyoitoa sambamba na kuonyesha bango juu.

“Sisi tumewaelewa. Tuwaachie madaktari wafanye kazi yao katika hospitali aliyopo. Nina hakika kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu, kupitia jitihada zao, watafanikiwa kumpatia huduma nzuri, itayorejesha afya kuwa kama awali, ndipo sheria ichukue mkondo wake,” alisema Mkuu wa jeahi la polisi Mangaka (IGP) Ibrahim Kachoti, pindi akiongea na mamia ya watu waliokusanyika katika uga wa Makao makuu, punde baada ya vurugu kumalizika.



Kidogo! Kauli hii iliwapa fariji. Si kwa hawa waliokusanyika makao makuu pekee, hapana. Bali hata wale wa mjini Lukwika pia. Hali iyowashawishi wasitishe vurugu kisha kusubiri, hali ya mgonjwa inaendaje.

“Endapo palepale hospitalini akifa, haina shida. Ila akitoka mzima! Hamna kupoa, hatua kwa hatua mpaka kieleweke,” alisema mmoja wa waandamanaji akimwambia mwenziye pindi wakirejea makwao.

“Yeah! Yatupasa kufanya hivyo. Maana hamna namna nyingine zaidi ya hiyo.”



Hali haikuwa shwari kwa makamanda wakuu wa majeshi, na idara zingine za ulinzi na usalama. Mara kwa mara hawakuacha kukutana kujadili mustakabali wa hilo, kiasi kwamba, ilifikia siku, walisafiri usiku usiku kuelekea mjini Lukwika kuthibitisha mtu aliyopo hospitalini kuwa ni james ama lah! Ila cha kushangaza, juu ya uthibitisho dhahiri, walioshuhudia kwa macho yao, Mkurugenzi wa usalama wa Taifa, Knl. Mstf. Faidha Mwembere, alipinga. Kuwa huyo sio James, bali kafanana naye tu. Kuwathibitishia, pingamizi lake, aliwasiliana na Mkuu wa kitengo cha PSS, Zaulyn Mwakibunda, kwa njia ya video call kupitia simu kisha kumuunganisha mmoja wa vijana waliomtengeneza kuwa James. Kwa kutumia sura bandia.

“Yule ndiyo James wetu, huyo mnayemsema hatuhusu. Yumkini wamefanana tu, ama katengeneza sura bandia ili amchafulie,” alisema Mkurugenzi wa usalama wa Taifa, Knl. Mstf. Faidha Mwembere, walivyokutana wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama, katika kikao chao cha mwisho cha dharura.

“Ila inaweza kuwa sahihi. Kwa hiyo tunaamuaje?” aliuliza Mkuu wa jeshi la ukombozi wa wananchi, Jenerali Umulisa Ngaeje. Mwanamama aliyewahi pata kuwa, Komandanti wa vikosi mbalimbali vya majeshi ya Umoja wa mataifa, yaliyokuwa yanashughulika kulinda amani nchi mbalimbali duniani kwa miaka takribani kumi na sita.

“Tusubiri apone. Baada ya hapo achukuliwe hatua, hamna cha ziada.”

“Yeah! Tukubaliane na hilo.”

“Wote tupo pamoja, ila aongezewe ulinzi. Uwe mkali na wa nguvu zaidi ya sasa.”

“Hilo lishapita.”



Kweli! Punde kikao kilivyohitimishwa, IGP Kachoti, akaamuru, kamanda wa polisi mkoani Michiga, aongeze nguvu ya ulinzi, kwa James, ambao nao tayari walishakubaliana na kauli waliyoambiwa na Mkurugenzi wa usalama wa Taifa. Hakuna hata mmoja, aliye na chembe ya hisia kuwa wanaongopewa. Agizo la IGP Kachoti, lilitekelezwa muda huohuo. Askari kadhaa, waliteuliwa, na kufanya idadi ya askari waliokuwa wanamlinda kufikia askari kumi. Ila walikuwa wanawekeana zamu. Si wote waliingia kazini pamoja. Idara ya usalama wa Taifa nayo (MIA) ilikuwa inatoa vijana kadhaa, kufanya doria ya kutembelea hospitalini hapo.



Wiki moja ilikata, unafuu ulionekana kuwa shida, na kukosa matumaini kwa James (Sadiki). Hali iliyochangia baadhi ya siku, uongozi wa hospitali na makamanda waandamizi wa majeshi kuangalia namna ya kumsaidia, ili fahamu yake irejee kwa haraka. Ambapo baada ya vuta nikuvute nyingi katika majadiliano yao, waliridhia, madaktari waliohusika mwanzo, na wengine pia wenye uwezo ambao mwanzo hawakuhusika wakutane hospitalini hapo kuchunguza wabaini tatizo ni nini linalopelekea kuchelewa kurejewa fahamu kwa James. Hilo lilienda sambamba, na upotevu wa mwili wa marehemu, Joram ama Mashaka kama alivyotambulika na wengi, ndani ya mji wa Lukwika. Askari kadhaa pia, wapatao wanne, walio ndani ya kikosi maalumu, kifahamikacho CRT (Cris response team) chenye ujuzi na mbinu mbalimbali za kimapigano, pia wabobezi wa uokoaji wa mateka, waliotekwa na kufichwa sehemu tofautitofauti. Kikosi hicho kiliongozwa na ASP Nendakulola, akisaidiwa na SGT. Zena Chaula, mpelelezi mahiri, mdunguaji na mtaalamu wa milipuko. Alifuatia CPL Malkiadi Makambo, mpelelezi na mtaalamu wa teknolojia. Wa mwisho, katika askari waliounda kikosi hicho ni PC Juma Makokola, mdunguaji tegemezi wa kikosi.



Kazi yao kubwa ya kwanza, waliyoifanya, ni upelelezi. Kufahamu kama huyo mtu ni marehemu ama tayari ni mzima. Hivyo walianza kupeleleza pale alipokuwa anaishi, baada ya hapo mazingira jirani, kisha walimalizia makaburini. Katika makaburi yapatikanayo ndani ya mji huo, kuchunguza kama kuna kaburi, linaloonekana mtu amezikwa siku za karibuni. Walizunguka mji wote, yale waliyoyaona, na kuyahisi, hayana muda mrefu, hata kama ni kaburi la mtoto mdogo waliliwekea kodoni, kisha kuendelea sehemu nyinginezo. Kwa lengo, siku za baadaye yafukuliwe, mabaki yatayopatikana yafanyiwe vipimo pamoja na vile vielelezo walivyovikuta siku ya tukio. Hawakuishia mjini pekee, walihamia na baadhi ya vijiji jirani, ambako asilimia kubwa, hutawaliwa na matukio ya uhalifu. Pasi na sahau misituni, wapendayo kutumia wahalifu.

“Tushamaliza kazi ya kwanza. Ifuatayo ni ufukuaji, hii tuanze kuifanya kesho. Ili tupate kupumzisha miili yetu, tukianza, tuanze na nguvu ya kutosha,” alisema Asp Nendakulola.

“Hamna shida afande, ni wazo jema, na ni zuri. Mimi nakuunga mkono.”

“Wengine vipi?”

“Hata nasi tupo pamoja nawe kwa hiyo kauli.”



Siku hiyo walipumzika, huku wakifanya maandalizi ya hapa na pale katika safari ya kuanza upya majukumu siku ya kesho. Hawakuhitaji kupoteza, sababu ni kikosi imara, kiaminiwacho, si kwa Lukwika pekee, hapana! Bali kwa Taifa zima. Kwani ni hawahawa ndiyo miongoni mwa kikosi kiundacho CRT ya Taifa, kijumuichasho askari toka miji tofautitofauti.

****



WanaPSS, wale walioko nchini Msumbuji, nao walikuwa bega kwa bega kufuatilia kila kilichokuwa kinaendelea nchini mwao. Mangaka! Jambo lililowapa sintofahamu kwa kiasi kikubwa, walivyosikia kilichomsibu James. Mtu waliyemwaminia na kumpenda sana, kutokana na utendaji wake wa kazi. Kilichotokea kiliwapa hasira, hata kiongozi wao anayewaongoza pia, alikasirishwa. Na kuwafanya jioni moja wamvae Rais, Ndg. Mohammed Mlunji, ambaye naye alikuwa na taarifa kuhusu kiendeleacho. Awaeleze kafanya nini kwa James hadi akumbwe na masaibu ya aina hiyo.

“Tuambie mkuu, umemfanya nini mwenzetu? Hadi leo hii yupo kwenye matatizo kiasi hiki. Ambayo katu hawezi yakwepa,” aliuliza kiongozi wa wanaPSS, Zaulyn Mwakibunda.

“Hamna chochote, nilichomuagiza afanye. Mimi nilimpatia likizo tu ya muda, akishamaliza kazi yake arejee kazini. Sasa kama kaenda huko, kisha kajihusisha na mambo mengine, hayanihusu,” alisema Rais Mlunji. Ilibidi awaongopee, ili asichukiwe na wanausalama, na wananchi pia endapo wakipata taarifa kahusika kwa namna moja ama nyingine katika kile alichokuwa anafanya James.

“Kama ni hivyo, kwanini kafanya mambo ya kijinga? Ama kasingiziwa?”

“Yote yanawezekana. Kufanya ama kusingiziwa. Tusubiri, akipona tutafahamu ukweli.”

“Kwa sheria ya idara yetu, sina hakika kama ataweza ru……….!” alisema Zaulyn, ila hakuweza malizia kauli yake, Rais Mlunji, alimkatisha.

“Nafahamu!”



Mambo yalienda sivyo, kama Rais Mlunji alivyotaraji. Na hakuwa na mbadala zaidi ya kumkana James, ili wabaya wake wasitumie mwanya huo kuzidi kumdhorotesha. Alifanya, lakini roho ilikuwa inamuuma sana, kwanini kamsaliti kijana wake hodari, amuaminiaye. Alivyomaliza maongezi na wanaPSS alirejea chumbani kwake. Alivuta moja ya begi lake dogo alilohifadhi nyaraka mbalimbali. Alivyolisogeza jirani naye, alilifuta vumbi kisha alilifungua. Alichambua, bahasha na karatasi nyingi, zilizo wazi zingine zilizo kwenye mafaili, alivyofika mwisho, chini ya begi, alitoa simu ndogo ya mkononi, iliyo na mkonga. Aliiwasha, akafuatia kubonyeza vitufe kadhaa, baada ya hapo aliisogeza katika moja ya sikio lake. Haikuchukua sekunde nyingi, kuwa kwenye maongezi na mtu wa upande wa pili.

“Dokta!” aliita Rais Mlunji.

“Ndiyo mkuu.” Alisema mtu wa upande wa pili wa simu.

“Nakutegemea.”

“Ondoa shaka. Kwani hamna kitachoharibika.”



Simu ikakatwa. Na kurejeshwa begini, baada ya hapo alilirejesha begi sehemu alilopolitoa.

Mikakati, kanuni, taratibu na sheria za usalama wa Taifa, hazimtaki mtumishi yeyote wa idara hii kujihusisha katika mambo ya uhalifu wa waziwazi, ubainikao kwenye jamii. Kufanya hivyo, mtumishi huyo, abainikapo, haraka sana huchukuliwa hatua, ya kufukwa kazi, ama kubadilisjwa jina lake (Kuuwawa). Kwani asilimia kubwa, wakuu huamini, akifukuzwa, mtaani ataenda toa siri za idara, sasa ili zisivuje hatua ya pili hutumika zaidi ya hatua ya kwanza. Pasi na huruma, takwa hilo la kisheria hutumika. Tena kwa haraka mno, kabla mambo hayajaharibika zaidi.



Ufahamu wa sheria hiyo, ndiyo uliwafanya, wanaPSS kumvaa Rais Mlunji, wafahamu ukweli kuhusu James, kwani walifahamu fika, hana maisha marefu mbeleni. Ataenda kuuwawa na watu wa idara wenyewe, idara isichafuke kwa jamii. Awali walikuwa na wingi wa huruma, ila walivyoongopewa, na kuaminishwa kile kilichotokea ni mambo yake binafsi, huruma yote iliwaisha, na kujawa subra, ya kuona nini kitachojiri. Atauwawa ama atasamehewa. Wakati huo Mkurugenzi, Knl. Mstf. Faidha Mwembere, akili yake haikutulizana. Kumbukumbu nyingi, za maongezi aliyofanya na watangulizi wake waliokwishapita iongoza hiyo idara, hayakumwisha. Kila ayakumbukapo yalimuumiza akili na kumkosesha furaha na amani ya moyo wake.

“Kijana wako akiharibu, kiasi kwamba jamii ikatambua, basi hautafaa kuitwa kiongozi. Fanya uwezavyo kuhakikisha hili halikutokei. Iga mfano toka kwetu, uitwe hodari, shujaa na majina mengi yenye neema,” alikumbuka Knl. Mstf. Faidha, akiwa ameketi ofisini kwake. Kauli alipata kuambiwaga na mtangulizi aliyetoka badala yake, Kapt. Maguta Mustafa.

“Acha sheria ifuate mkondo wake,” alijikuta anaropoka kwa nguvu.



Muda huohuo alivuta simu yake ya mkononi, aina ya Sony Ericson, alibonyeza vitufe kadhaa na kuweka sikioni.

“Mkataba upo mezani,” alisema Knl. Mstf. Faidha, punde simu ilivyopokelewa na mtu wa upande wa pili.

“Hamna shida kiongozi. Sitokuangusha,” alijibu yule wa upande wa pili.



Hayakuwa maongezi marefu, alikata simu na kuunga kwa mtu mwingine. Naye kumwambia maneno yaleyale aliyomwambia mtu wa mwanzo. Alivyokata aliirejesha alipoitoa na kutulia.

“Samahani James, hamna njia ya kuisaidia idara yetu, na wewe mwenyewe kwa ujumla zaidi ya hii inayoenda kukuta,” alijisemeza Kanali Mstaafu Faidha Mwembere kimoyomoyo.





Simu alizopiga zilitua kwa vijana wawili. Wafahamikao, Hussein Kalumbwe, mtaalamu wa teknolojia, mdunguaji na mtumishi ndani ya idara kongwe ya usalama wa Taifa. Mwenziye, akitambulika kwa jina la Aisha Makusega, mdunguaji, mwanafunzi wa chuo kikuu cha Lidede, mwaka wa pili, akisomea shahada ya sheria na ni mwenyekiti wa umoja wa wanawake wa chuo wa chama cha Maliga. Chama pinzani. Pia ni afisa wa Usalama wa Taifa. Alitumbukizwa ndani ya chama pinzani kwa sababu maalumu. Kudukua taarifa zote za siri zipangwazo na wakuu wa chama hicho kisha kuzifikisha serikalini na chama tawala kwa ujumla. Hawa ndiye, watekelezaji wakuu, wanaoaminika, katika shughuli ya namna hiyo, waliyokabidhiwa. Kila mmoja alifanya maandalizi yake, kabla hawajaenda fanya maandalizi ya pamoja watavyokutana. Walivyotayarika, waliondoka makwao na kwenda kukutana katika hoteli moja iliyoko nje kidigo ya mji wa Lidede. Huko waliweka mikakati yote, namna itavyokuwa hadi wafanikishe kile walichoagizwa. Namna pekee, waliyokubaliana, ya awali; ni kujifanya madaktari waliyoarifiwa waelekee mjini Lukwika kwenda kushughulikia tatizo la fahamu linaloendelea kusumbua. Ambapo walipanga, kuwasitisha wale madaktari wa mbali waliotakiwa kwenda. Kisha wao kuchukua nafasi hiyo badala yao. Hivyo chapchap, waliomba mawasiliano ya hao wahusika. Akiwemo Dkt. Kanyunya. Mmoja wao, akapiga simu kwa mkuu wao. Kanali Mstaafu Faidha, kisha kueleza hitajio walilojipangia. Ambalo walitekelezewa sekunde chache baada ya kukata simu. Walitumiwa mawasiliano ya kila mmoja, namba ya simu, anuani ya barua pepe na ile ya faksi. Muda huohuo walianza kuwasiliana nao. Kwa njia ya barua pepe. Waliandika ujumbe nzuri, ulionekana umeandikwa na kiongozi mmoja wapo wa hospitali ya Lukwika, ukiwataka kusitisha safari zao, kwa madai James ashaonesha dalili zote za kuamka. Kisha wakatuma kwa kila mmoja.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Sasa kwa hiyo njia si watabaini mtu gani katuma?” aliuliza Aisha.

“Hapana! Hawawezi baini kama huo ujumbe ni wa kugushi, maana nimetengeneza anuani inayoonyesha sisi ndiyo uongozi wa hospitali ya Lukwika, kisha ile yenyewe ya hospitalini nimeizuia.”

“Umeizuiaje?”

“Nina maana kuwa nimeifunga. Hivyo haitotumika kwa namna yoyote ile.”

“Mmmmh! Hapo sawa. Na naamini tutakamilisha ndani ya muda mfupi tu,” alisema Aisha, huku wakitoa zana wanazopaswa kutumia kwa muda huo.



Walivua mavazi waliyovaa. Ya ujana, na kuvaa nguo zingine, zenye heshima na hadhi stahili ambazo hukubaliwa na mtu yeyote. Walivaa suti nzuri, nyeusi, zenye mng’ao kisha kufanya mabadiliko kadhaa ya sura zao. Walivyojihakikisha wako sawa, hawawezi bainika, walianza safari ya kuelekea mjini Lukwika. Mioyo yao ikijaa matumaini, kwamba hawatochukua muda mrefu, kukamilisha kazi hiyo, kwa sababu si mara ya kwanza kutekeleza, na tangu waanze kutekeleza hawajawahi kufeli. Awamu zote hufanikiwa. Walisafiri kwa ndege, ndogo ya kukodi, hivyo iliwachukua dakika arobaini na tano kuwasili mjini Lukwika. Kwa kuwa kazi yao iliwafanya kuwa na vitambulisho vingi, vya kila aina, vilivyowaonyesha wao ni wakubwa katika idara, hali iliyochangia, kwao, mwiko kukaguliwa. Walivyoteremka ndani ya ndege, walivyoonyesha hivyo vitambulisho tu, hawakuguswa, waliachwa, wakaondoka zao. Walivyofika nje, waliita taksi. Na kumuomba dereva, awapeleke nje ya hospitali, hawakutaka kuingia moja kwa moja wodini. Walifanya hivyo ili wapate fursa ya kumalizia mambo waliyosahau kufanya kama yapo. Toka uwanja wa ndege hadi hospitalini ulikuwa mwendo wa dakika ishirini, huku barabarani wakipishana na gari ya wagonjwa, maeneo ya katikati, kati ya uwanja wa ndege na hospitalini, iliyokuwa mwendo mkali, ikumwahisha mtu, tena ikisindikizwa na ulinzi mkali wa askari polisi, waliobeba bunduki zenye risasi za moto. Walivyofika, waliteremka nje ya wigo, uliozunguka hospitali hiyo. Walimlipa dereva kisha taratibu, walianza piga hatua kuelekea ndani, huku wakiteta jambo.

“Vipi umeangalia kama washajibu hao uliowatumia ujumbe?” aliuliza Aisha.

“Hapana! Unawasiwasi kuwa hawajafikiwa?” alijibu Kalumbwe, huku akiingiza mkono wake katika mfuko wa suruali na kutoka na simu.

“Inaweza ikawa. Ujumbe haujawafikia, halafu wamekuja huku.”

“Sina hakika. Na nikuombe, usiruhusu hilo wazo akilini mwako. Tuombe, na tuzipe akili zetu, hisia za ushindi muda wote, kama mafunzo yetu yatutakavyo.”

“Sawa.”



Kalumbwe aliingia mtandaoni, kuangalia mambo ya hapa na pale kisha kuhakikisha, kama jumbe aliyotuma imejibiwa. Ila cha kushangaza, hadi kufikia muda huo hakuna mtu yeyote aliyejibu kati ya wote aliowatumia. Hakusita kumwambia mwenziye, na kuwafanya waingie kwenye majadiliano ya kina pasi na matarajio, wakiwa wamesimama kwenye lango kuu la kuingilia uga wa hospitalini hapo. Walitumia takribani dakika nne, ndipo walipata muafaka, uliowahimiza wasonge mbele. Wasikate tamaa.

“Twende tu, tutafahamu hukohuko. Wakijifanya kuhojihoji sana, tutawaambia nasi tumepewa amri toka wizarani ya kuja kuongeza nguvu.”

“Tutatolea wapi nyaraka yoyote ya kuthibitisha hiyo kauli?”

“Ondoa shaka, upo na mwanateknolojia. Hamna kitachoharibika,” alisema Kalumbwe, huku akijitunishatunisha misuli, kuonyesha yeye ni mwamba.



Hatimaye walisonga mbele, na kuifikia ofisi ya Mganga Mkuu. Walibisha hodi, kwa kidole kimoja wapo kugonga mlango, ilivyoitikiwa, waliingia. Walivuta viti wakaketi, baada ya hapo walitakiana hali, kisha maongezi mengine yalifuata. Ambayo ni ya utambulisho na mengineyo.

“Sisi ni madaktari toka hospitali ya Mt. Likungwa iliyopo mjini Lidede. Tupo hapa kutii wito, wa wizara tuliopatiwa juzi, kuja kuungana na madaktari wengine katika kumhudumia James,” alisema Kalumbwe, kauli iliyoambatana na zoezi la utoaji bahasha katika begi lake dogo. Bahasha iliyobeba barua iliyowatambulisha wao ni watu gani.



Mganga Mkuu alivyoipokea, hakuchelea, aliifungua bahasha, akatoa barua na kuanza isoma. Kweli! Barua ilionekana toka wizarani, ilhali ni ya kughushi, iliyobuniwa na Kalumbwe. Wala haikutiliwa shaka, kwani iliendana na barua zingine ziletwazo toka wizarani. Naam! Ilileta uaminisho mkubwa mno kwa Mganga Mkuu. Tena alivyoomba kuoneshwa vitambulisho vyao, majina yalioana na yale yaliyopo baruani. Alivyojiridhisha alivuta pumzi kidogo kisha aliziachia. Aliangaza macho yake kwa wote, akayarejesha baruani, baada ya hapo alijikohoza kidogo, na kuanza zungumza.

“Ndugu zanguni, mambo yameharibika.”

“Kwanini unazungumza hivyo?” aliuliza Kalumbwe, macho pima kwa Mganga mkuu, kumuona namna atamkavyo maneno.

“Nusu saa iliyopita, nimepokea barua toka wizarani pia, iliyotuhitaji tumsafirishe mgonjwa kumpeleka hospitali ya taifa,” alisema Mganga Mkuu huku akiwaonyesha barua aliyotumiwa.

“Ina maana James hayupo hospitalini kwa sasa?”

“Swadakta! Ninyi nyote mnapaswa kuelekea hospitali ya taifa.”



Aisha na Kalumbwe waliduwaa. Nguvu ziliwaishia. Ila hawakutaka kujionyesha dhahiri, lakini ndani ya mioyo yao ilijaa manung’uniko, na hasira kali, kwanini waliyemfuata kaondolewa. Kimya kidogo kilipita. Wakionekana kuwa kwenye tafakuri, kila mmoja kwa namna yake.

“Itakuwa ni ile gari tuliyopishana nayo pindi tunakuja huku,” aliwaza Kalumbwe. Akionekana kuguswa sana na kitendo hicho.

“Mmmh! Ni ile gari tuliyopishana nayo wakati tunakuja ama?” Aisha naye aliwaza.



Sauti ya runinga ndiyo iliwashtua, toka mawazoni. Iliyofungwa juu ukutani mwa chumba hicho cha Mganga Mkuu. Iliyowashinikiza kila mmoja kuongoza macho yake kule sauti ilikosikika. Ambapo sura ya mdada mrembo, ilipamba skrini. Aliyevaa mavazi nadhifu, yatumiwayo zaidi na wanawake wa kiislamu. Chini, ilipoishia picha yake, ulipita mstari mkubwa mwekundu, ulio na maandishi meupe yaliyosomeka ‘Breaking News’ umakini ulitawala, kwa kila mmoja, tena mtangazaji alivyoanza zungumza ndiyo walizidi. Hata kutingishika hawakuruhusu, walihofia kupoteza uhondo.

“Gari ya wagonjwa iliyokuwa inamwahisha mgonjwa uwanja wa ndege, kuwahi ndege yashambuliwa kwa risasi. Na askari polisi, wasindikizaji wa gari hiyo watekwa na kupuliziwa sumu iliyowafanya wasijitambue kwa muda. Tujiunge na ripota wetu toka Lukwika kwa habari zaidi,” ilisikika sauti ya dada huyo, punde picha yake ilivyotoweka, ilifuatia picha ya video iliyorekodiwa muda wa dakika moja, ikionyesha tukio.





Walistaajabu, walipigwa na butwaa, na mshawasha wa hali ya juu uliwapanda. Kutaka kufika eneo la tukio kushuhudia bayana kiendeleacho.

“Aaaah! Hapa ni pori la Mtalikachau, pori liunganishalo hospitali ya mji wa Lukwika na uwanja mdogo wa ndege wa mji huo, hali si shwari, baada ya gari la wagonjwa kushambuliwa kwa risasi zipatazo tano, kisha kupoteza uelekeo na hatimaye kugonga mti. Tukio lililopelekea watu waliomo ndani, dereva, daktari, askari na muuguzi mmoja, kudhurika vibaya mno, achilia mbali mgonjwa, ambaye mpaka sasa haifahamiki wapi alipo. Uashirio kwamba, aidha mgonjwa huyo katoroshwa ama katoroka mwenyewe.”

“Gari hiyo ilikuwa chini ya usindikizaji wa askari polisi wawili, walio na bunduki zenye risasi za moto, ila isivyo bahati, askari hao wameshindwa kutumia zana zao, na hatimaye, kujikuta wamewekwa hatiani kwa kufungwa kudu, kisha silaha zao kutupwa umbali mdogo na wao walipo. Ni tukio la kusikitisha, na lenye sintofahamu kubwa, haijawahi tokea, hii ni mara ya kwanza, hivyo haina budi kuendelea kutega sikio kusikiliza kiendeleacho,” ilisikika sauti ya mtangazaji aliyoko eneo la tukio.



Kutoonekana kwa mgonjwa aliyekuwemo ndani ya gari ilimshtua kila mmoja. Ofisini mwa Mganga Mkuu hamukukalika tena, wazo la kwenda eneo la tukio lilivyoshika akili, mwishowe mmoja wao alilitoa bayana likakubalika. Dakika tatu baadaye, walishakuwa ndani ya gari, kuelekea kule ajali ilikotokea. Sio wao tu, hata wengine walioguswa walizuru eneo la tukio. Ambalo dakika nane zilikuwa nyingi, tayari lilikusanya zaidi ya watu mia mbili, waliokuja kwa ajili ya kushangaa na baadhi kutoa msaada. Watu wa vyombo vya dola, polisi, jeshi la ukombozi, wakiongozwa na makamanda wao wa mikoa, nao waliwasili na kuwa mstari wa mbele katika kusaidia. Hawa ndiyo walikuwa mstari wa mbele katika utafutaji, tena walivyopenyezewa taarifa na mmoja wa madaktari waliopo kuwa mgonjwa aliyepotea ni James, walipandisha midadi kumtafuta, na wale raia, waliojitolea walizuiawa kuendelea na utafutaji. Zoezi likabaki ndani ya majeshi, waliweka mikakati, iliyowataka hadi kufikia mchana wa siku inayofuata kuwa na taarifa tosha kuhusu huyo aliyepotea. Wengine, raia. Walirejea makwao, ila si kwa mapendo, walishinikizwa kuondoka ili siri isivuje. Kwa Kalumbwe na Aisha, wao walizunguka mlango mwingine, walibadili mavazi na kuingia kazini nao kumtafuta kwa namna wajuavyo wao, huku wakijiweka mbali na vyombo vya majeshi vilivyopewa jukumu la kutafuta. Watu wa majeshi walipita huku wao kule, lengo wasibainike. Muda mwingine waliwafuata nyumanyuma, kusikilizia mikakati wanayoendelea nayo.

“Afande! Afande! Afande!...kuna vitu tumebaini hapa, nadhani vilikuwa mwilini mwa mgonjwa,” alisikika askari mmoja toka jeshi la polisi, alivyoona bandeji zilizolowana damu na sindano zilizo na mishipa ilioonekana kutumika kupitishia damu kuingiza mwilini, vimelundikwa sehemu moja.



Wote waliosikia kauli hiyo walifuata sauti ilikosikika. Walivyofika, walishuhudia kila kilichopo, na walivyoangaza kwa makini, waliona nyayo za buti, zilizowahimiza kuzifuatilia. Walizifuatilia zilikoelekea, moja kwa moja, wakaishia, barabarani. Barabara inayounganisha mji wa Lukwika na Lumesule, upande wa pili ukitawaliwa na pori kubwa lililowakatisha tamaa kulihisi kama wamtafutaye kaingia huko.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Inavyoonekana, alivyofika hapa, alisubiri usafiri.”

“Sahihi! Tena wa kumpeleka Lumesule, na si Lukwika.”

“Pana umbali gani, toka hapa kuelekea Lumesule?”

“ Takribani saa tatu.”

“Na usafiri wake ukoje?”

“Zipo gari tatu, zielekeazo huko. Moja hupita asubuhi, mchana na nyingine jioni.”

“Kwa hiyo ya mchana itakuwa ishapita.”

“Ndiyo. Tena kwa sasa nadhani gari itakuwa kijiji kifuatacho hapo mbele kiitwacho Nandete.”

“Haina haja ya kuchelewa. Wapewe taarifa askari waliopo barabarani waisitishie safari hiyo gari kabla haijafika Lumesule,” aliamuru kiongozi wa oparesheni, ambaye alikuwa ni Luteni toka jeshi la ukombozi.







ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog