Search This Blog

Saturday 5 November 2022

SAUTI YAKE MASIKIONI MWANGU - 1

 




IMEANDIKWA NA : KELVIN KAGAMBO



*********************************************************************************



Simulizi : Sauti Yake Masikioni Mwangu

Sehemu Ya Kwanza (1)







“..... na sasa ni zamu yako. Sali sala za mwisho tufunge mkataba.”



“Lakini braza Jisu haya yote yanatoka wapi? Kosa langu nini?”



“Unaleta dharau sio? Hujui kosa lako au unauliza kutafuta faida? Sikia Mkuki, mimi sio Jisu yule unayemfahamu, halafu hii kazi ni lazima itimie, lazima nikuue.” Akazungumza kwa msisitizo mwanaume huyo aitwaye Jisu; mrefu, mweusi mwenye mwili wa mazoezi; upara kichwani na sharafa nene zilizoungana kidevuni kutokea chini ya kila sikio lake.





Kisha akaikamata barabara bastola iliyokuwa mkononi mwake, akamuelekezea Mkuki ambaye kwa muda huo alikuwa amepiga magoti mbele ya Jisu. Akavuta pumzi zake kwa kuhesabu moja mpaka tatu ili kujiongezea ujasiri. Akatumbukiza kidole cha shahada cha mkono wake kwenye ‘trigga’ ya bastola kisha akaanza kubofya taratibu.



“Paaaaa!” Mlio mkubwa wa risasi ulisikika nama hiyo, lakini kabla hata shambulio hilo halijafanikiwa Mkuki alikurupuka kutoka usingizini na kuikata ndoto ile mbaya yenye kutisha.



Akaketi kitandani huku akitweta na kutokwa jasho mithili ya mtu aliyelowa mvua ya manyunyu. Akajipa sekunde kadhaa kuirejesha akili yake duniani na alipofanikiwa katika hilo alishusha pumzi ndefu ya kushukuru kwamba lile halikuwa tukio halisi.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Ghafla akashituka; aligundua kitu kipya ambacho hakikuwa cha kawaida—aling’amua kwamba alikuwa kwenye chumba asichokifahamu kabisa, yaani hakuwahi kuwa hapo kabla.



Kilikuwa ni chumba chenye ukubwa wa chumba cha kawaida cha kulala, kuta zote za chumba hicho zilipakwa chokaa huku kitanda na meza ndogo vikiwa ni vitu pekee vilivyomo ndani.



‘Niko wapi?’ Likawa ni swali la kwanza kugonga kichwani mwa Mkuki. Hapo akajipa muda kuvuta kumbukumbu ya kila alichopitia kabla ya kuwa pale chumbani na hakika ubongo wake ulimsitiri, alikumbuka kila kitu.



Alikumbuka watu wawili aliokuwa nao mara ya mwisho, akakumbuka ajali mbaya aliyoipata akiwa na watu hao, pia alikumbuka kwamba ajali ile ilisababishwa na mlipuko mkubwa wa bomu.



‘Au nimesaidiwa?’ akajiuliza Mkuki ‘Lakini ngonja, ngoja nione.’ Akajipa  moyo wa kusubiri na hamasa ya kufanya udadisi.



Basi akateremka kutoka pale kitandani; alihisi maumivu mwilini lakini hayakumzuia kutembea kuelekea mlangoni. Lakini kabla hata hajafikia lengo mlango ulifunguliwa, akaingia mwanamke mmoja aliyekuwa akiimba kwa sauti ya juu iliyoashiria uhuru mkubwa alionao, lakini ghafla mwanamke huyo aliacha kuimba mara tu alipomuona Mkuki.



Alikuwa ni mwanamke wa ki-Asia, msichana mfupi, mwembamba, mweupe mwenye nyelwe ndefu na nyingi zilizoficha uso wake wote ingawa hilo halikumzuia kuona mbele.



“Umeamka?” Akauliza mwanamke huyo, lakini kwa lugha ambayo Mkuki hakuilewa, lugha yenye kufanana kabisa na Kichina.



“We ni nani?” Mkuki naye akamtupia swali kwa lugha adhimu ya Kiswahili huku akirudi nyuma taratibu.



“Tulia. Kaa kitandani.” Yakamtoka  kwa upole yule msichana, tena kwa lugha ile ile yenye kukanganya masikioni mwa Mkuki.



“Wewe nani na niko wapi hapa?”



“Tulia. Rudi kitandani. Bado hujapona, utajitonesha.” Akasema msichana huyo lakini kwa sababu ya mgongano wa lugha kati yao ilikuwa ni kama anatwanga maji kwenye kinu.



Akanyamaza kidogo yule msichana, akamtazama Mkuki kana kwamba kuna kitu alikuwa akifikiria juu yake kisha akapaza  sauti kumuita mtu ambaye bila shaka hakuwa mbali na chumba kile.



“Babaaaa....” Aliita hivyo na sauti ya kiume kutoka nje ikamuitikia.

“Njoo. Amaeamka.” Akasema binti.



Punde mlango ukafunguliwa, akaingia mzee ambaye kwa mtazamo wa haraka Mkuki alijiridhisha kwamba babu huyo alikuwa ni Mchina. Alikuwa ni mzee wa kati ya miaka 60 na 70; mfupi, mwembamba, mweupe, mwenye mvi kichwa kizima na macho madogodogo ya kuvimba.



“Umeamka?” Akauliza mzee huyo kwa lugha ile ile iliyokuwa ikitumiwa na yule msichana, kisha kabla ya kupewa jibu alimfuata Mkuki, akamshika mkono na kumchukua hadi kitandani, akamkalisha.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



“Unajisikiaje?” Akauliza yule mzee lakini kwa jinsi ambavyo Mkuki alikuwa akimtazama akagundua fika kwamba kulikuwa na kikwazo cha lugha kati yao.



“Hunielewi? Huzungumzi Kithaiwan?” Akamuuliza lakini bado aliambulia jibu la ukimya.



Akamgeukia yule msichana. “Haelewi.” Akamwambia. Kisha akamgeukia tena Mkuki. “Unaitwa nani?” Akamuuliza; hapa akijitahidi kutumia na vitendo kutafsiri swali lake.



Mkuki akamuelewa lakini pia tayari alishagundua kwamba watu wale hawakuwa na lengo baya juu yake.



“Mkuki. Naitwa Mkuki.” Akajibu.



“Nani?.”



“Mkuki.” Akajibu kwa msisitizo.



“Mkuki?” Akauliza yule mzee kuthibitisha.



“Ndiyo.” Akajibu huku akitingisha kichwa kukubali.



“Ooooh! Mimi ni Wong,” akajitambulisha yule mzee na kuongozea. “Na yule ni Mei Lee.” Akamtambulisha na yule msichana.



“Sisi tumekuokota ufukweni. Tumekusaidia. Unaweza kutuambia unatokea wapi?” Akahoji yule mzee lakini Mkuki alibaki akitumbua macho tu kama ishara ya kwamba hakuwa akimulewa, labda tu pale alipojitambulisha yeye pamoja na yule msichana.



“Baba? Hakuelewi. Tumpe muda.” Akazungumza yule msichana ambaye muda wote sura yake ilikuwa imefunikwa kwa nywele zake ngingi na ndefu.



“Sawa. Simama. Twende.” Akasema yule mzee aliyejitambulisha kwa jina moja la Wong huku akisindikiza sentesi yake kwa vitendo, Mkuki akamuelewa, akasimama na kuanza kumfuata kuelekea nje.



**************************************

Mkuki Salum Goigoi ndilo jina lake halisi, kijana aliyezaliwa na kukulia nchini Tanzania. Hadi mwaka huo 1998 alikuwa na umri wa miaka 23 duniani ingawa haikuwa rahisi kugundua hilo kwa kumtazama; alikuwa akionekana mkubwa zaidi na amekomaa kwelikweli.



Ni mwembamba wa kukonda, mrefu, mweusi mwenye uso wa duara wenye kufanyiza upole fulani unapomtazama; ingawa si kweli kwamba amejaaliwa haiba hiyo.



Kichwa chake kilibeba kumbukumbu za yote yanayomuhusu; yaani alipotoka; kilichotokea; yeye ni nani na mengineyo lakini juu ya yote hayo alinuwia kutowaambia wenyeji wake ukweli wowote na hii ni kwa sababu alikuwa anataka kukwepa kurejeshwa nchini Tanzania.



Hapo alikuwa nchini Thaiwan; taifa dogo ambalo ardhi yake yote ni kisiwa.  Nchi ambayo ipo barani Asia, katikati ya China na taifa la Taiwan.

Wathaiwan walikuwa wakifanana kwa kiasi kikubwa sana na Wachina; kimuenekano, kitamaduni na hata itikadi. Wenyeji wa Mkuki walikuwa wakiishi Mkoa wa Shenghei katika kijiji kiitwacho Chensuua; kijiji ambacho wakazi wake walikuwa wakiishi kwa kutegemea shughuli za uvuvi kwa kiasi kikubwa.



Basi kwa siku chache za awali Mkuki aliishi na wenyeji wake kama mtu asiyekumbuka lolote; alijitengenezea mazingira hayo ili wenyeji wake wasipate sababu ya kumrejesha alipotoka; lengo lake ilikuwa ni kulowea palepale.



Kwa siku tano tu za awali alitambulishwa kwa vijana wenzake; kazi hiyo aliifanywa na mzee Wong ili kumsaidia Mkuki kujifunza jinsi ya kuishi kwa kuendana na taratibu zao za maisha ikiwemo kuifahamu lugha kwa urahisi na mambo mengine.



Katika hilo Mkuki alipata changamoto kubwa ya ubaguzi; yaani ingawa vijana walimkubali wakati anatambulishwa kwao lakini hawakutaka kuwa karibu naye—hilo lilifanywa nyuma ya mzee Wong, walimbagua Mkuki kwa sababu ya rangi.



Lakini Maufeng aliamua kuwa tofauti ya vijana wote wa kijijini Chensua—huyu yeye alikuwa ni mvualana wa Kithaiwan ambaye ni pekee aliyekubali kujenga ukaribu na Mkuki ingawa pia kulikuwa na sababu iliyomsukuma kufanya hivyo.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



Maufeng yeye alikuwa na matatizo ya akili yanayompelekea kuwa mwendawazimu kabisa kwa kipindi fulani, hivyo vijana wengi walimtenga pia ingawa tatizo lake halikuwa likitokea mara kwa mara.



Maufeng akawa ni mtu wa tatu muhimu kwa ajili ya maisha ya mkuki pale ugenini, yaani ukiwajumuisha mzee Wong na binti yake Mei Lee.



******************************



Wiki mbili za Mkuki ndani ya Thaiwan zilikatika. Sasa taratibu alionekana kuanza kuifahamu lugha ingawa si kwa kiasi kikubwa, na msaada wa nguvu aliupata kutoka kwa Maufeng na mzee Wong, lakini Mei Lee—yule binti wa mzee Wong hakuwa katika orodha hiyo.



Ukweli ni kwamba Mei Lee hakuwa ni msichana wa kawaida; alikuwa ni mpole na kimya kupita maelezo na ili kuthubitisha hiko fikiria suala hili, kwamba tangu Mkuki aanze kuishi kwao hawajawahi kukaa pamoja na kupiga soga ingawa wote walikuwa ni vijana wanaorandana umri. Wala Mei Lee hakuwa na rafiki, jambo pekee alilokuwa akilifanya muda mwingi ni kuimba nyimbo zake mwenyewe na hakika alikukuwa ni mwanamuziki mzuri aliyejaaliwa sauti murua.



Yote tisa; kubwa zaidi ni kwamba kwa kipindi chote hicho cha wiki mbili cha Mkuki kuwa pale hakuwahi kuona sura ya binti huyo, muda wote aliifunika kwa nywele zake kama mtu anayeficha kitu fulani.





Kuna kipindi Mkuki alitamani sana kuuliza juu ya suala hilo la kuficha uso kwa nywele lakini hakuona hekima ndani yake; yaani angeazaje kuuliza kwa mfano?.



Hata hivyo baadae alipata mbadala wa hilo, alionelea ni vyema amuulize rafiki yake Maufeng kama anataka kujua ukweli, na alifanya hivyo kwenye mazungumzo yao ya kawaida.

“Kwanini Mei Lee anaficha uso kwa nywele?” Alitumbukiza swali la hivyo  katikati ya mazungumzo yao.

“Kwanini unaniuliza?” Maufeng akahoji.

“Nataka kujua au kumjua.”

“Unataka kumjua au unataka kunijua mimi kupita Mei Lee?”

“Sijakuelewa.”

“Namaanisha ni vyema ungeenda ukamuuliza mwenyewe.”

“Nitaanzia wapi? Hajawahi hata kukaa na mimi kuongea.”

“Wewe umewahi kukaa naye?”

“Hapana.”

“Kwanini?”

“Anaonekana hapendi ukaribu.”

“Labda na yeye anona huna ukaribu.”

“Hapana... sawa kama ni hivyo mbona hana hata rafiki?”

“Sio lazima kuwa na rafiki. Kama wote wanaokuzunguka hawajatimia vigezo vya kuwa rafiki zako kwanini uwe mnafiki?” akajibu Maufeng na kuuliza swali ambalo lilimfanya Mkuki atulie wakati likiingia ndani, kichwani taratibu.

Akaendelea Maufeng.

“Mimi namjua Mei Lee. Nimewahi kumuona na nina uwezo wa kuwa na jibu la kila swali lako kuhusu yeye. Lakini ukimuuliza mwenyewe utajua mengi zaidi. Jenga ukaribu naye kama kweli unatamani kumfahamu.".

******************************

Sasa Mkuki akajipa mtihani mpya, alinuwia na kujihakikishia kwamba ni lazima afahamu kwanini Mei Lee alikuwa akifunika uso wake kwa nywele lakini pia kujenga ukaribu naye zaidi kama ingewezekana.

Akiwa mbioni kuelekea lengo alilojiwekea, mzee Wong alimletea habari mpya. Alikuwa amemtafutia mtu wa kumfundisha uvuvi ili aweze kupata shughuli itakayomsaidia kujimudu kwa kipindi chote ambacho ataendelea kuwa pale hadi hapo kumbukumbu kuhusu nyumbani kwao zitakapomejea.

“Mtu atakayekufundisha ni mvuvi mzuri tu. Atakueleza na bila shaka utelewa ndani ya muda mfupi.” Alisema Mzee Wong na kuongeza, “Unajua sitaki ukae bure tu, nataka ujichanganye zaidi na vijana wenzako. Hii itasaidia hata kwenye kuiweka sawa afya ya ubongo wako.”

Basi baada ya mazungumzo hayo Mkuki alikutanishwa mara moja na mtu aliyepewa jukumu la kumfundisha na wakafikia makubaliano ya kwamba kesho asubuhi aanze.

Jioni ya siku hiyo alikutana na rafiki yake Maufeng na kumueleza mpango ule; swahiba wake alimuunga sana mkono huku akimuahdi kwamba mara baada ya kufuzu mafunzo hayo yasiyo rasmi wataungana na kuanza kufanya uvuvi pamoja.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Asubuhi ya mafunzo Mkuki aliamka mapema sana kwa ajili ya kujiandaa na yote hiyo ni kwa sababu alikuwa na nia ya dhati ya kufanya jambo lile. Nia aliyokuwa nayo ilitengenzwa na ile siri yake; siri ya kwamba alikukuwa akikumbuka kila kitu kuhusu wapi ametoka. Aliamini kwamba endapo atakuwa na shughuli maalum ya kufanya itakuwa ni rahisi kwake kuendelea kuishi hapo wakati akaiendelea kupanga mipango yake fulani fulani taratibu.

Ingawa uvuvi haukuwa ni shuhuli nyepesi lakini Mkuki alielewa kwa muda mfupi mno; ndani ya wiki mbili tu alikuwa amekwiva kiasi cha kuweza kufanya shughuli hiyo mwenyewe bila usimamizi. Uzuri ni kwamba alikuwa akifundshwa kwa vitendo halisi, yaani alifunzwa kwa mtindo wa kufanya kazi kama msaidizi wa mwalimu wake.

Baada ya kuhitimu mafunzo hayo aliungana na swahiba wake Maufeng katika mchakato wa kutafuta mtumbwi mdogo kwa ajili ya kuanza kazi rasmi. Halikuwa zoezi jepesi lakini kupitia msaada wa mzee Wong walifanikiwa. Walipata mtunbwi wa kukodi;ingawa awali waliuchukua bila kulipia kwa makubaliano ya kwamba pindi watakapovua na kuuza samaki watalipa pesa hiyo.

Kazi ilianza mara moja na kwa siku za awali ilionyesha mafanikio kwa kiasi cha kuwapatia pesa za kulipia mtumbwi na kujikimu nyumbani.

******************************

Mkuki alitimiza miezi miwili ya kuishi nchini Thaiwan, na sasa yeye akawa ndiye muhudumu mkuu wafamilia. Alileta chakula nyumbani sanjari na mahitaji mengine muhimu na jambo hili lilimtengenezea ukaribu kidogo na Mei Lee kwa sababu ilibidi msichana huyo amuongeleshe Mkuki pindi anapohitaji pesa kwa ajili ya mahitaji madogomadogo ya nyumbani.

Naye Mkuki alijitahidi kutoichezea nafasi hiyo, alihakikisha kwamba ukaribu wake na Mei Lee unajengeka ingawa tamati hakufanikiwa kama ambabvyo alitamani; yaani ni sawa ukaribu kiasi fulani ulikuwepo lakini si kwa ukaribu wa kina kama ambavyo yeye alikuwa akihitaji.

Ilibidi sasa aombe msaada  kwa rafiki  yake Maufeng kwa sababu aliamini jamaa huyo alikuwa akimfahamu vyema Mei  Lee kwahiyo ingekuwa ni rahisi kwake kumpa ushauri wa mbinu za kutumia ili kuukuza ukaribu wake na msichana huyo na hatimaye afanikiwe kufahamu kuhusu kufunika uso wake kwa nywele.

“Labda umnunulie zawadi, anaweza akalainika, akawa rafiki yako.” Alishauri Maufeng.

“Zawadi gani sasa itafaa?” Mkuki  akauliza.

Maufeng akacheka kidogo kabla yay kujibu, “Una maswali ya kijinga sana. Zawadi kwa ajili ya Mei Lee unaniuliza mimi!”

“Lakini we ndo uliyenishauri kuhusu zawadi.”

“Ndiyo. Mimi ninachofahamu ni kwamba binadamu wote tunapenda zawadi; linapokuja suala la zawadi gani hilo ni jambo binafsi.” Akafafanua Maufeng na kuongoza. “Lakini unaweza kumnunulia cheni, cheni za jedi. Ni nzuri, wanawake wengi wanazipenda.” Akasema.

Cheni za jedi zilikuwa ni miongoni mwa vitu vyenye gharama ya kawaida ambavyo wanawake wengi wa Kithaiwan hasa waishio vijijini walikuwa wakivipenda. Zilikuwa ni cheni zinazotengenezwa kwa kutumia madini ya Jedi na mchanganyiko wa mawe mengine yenye kufanana na dhahabu kwa mbali.

Basi Mkuki alifanyia kazi ushauri aliopewa; alichanga pesa kwa siku mbili tatu na zilipotimia akaenda kwenye soko dogo linalotumiwa na vijiji zaidi ya vitatu vya eneo hilo, na akanunua cheni yay Jedi kwa ajili ya kumpa Mei Lee.

Sasa mtihani ukabaki kuwa ni jinsi gani ambavyo ataikabdhi zawadi hiyo; katika hili pia aliomba msaada kwa Maufeng.

“Si umchukue muende ufukweni na umpe mkiwa huko.” Akashauri Maufeng.

“Nitamwambiaje sasa?”

Akacheka Maufeng. “Umeeanza na maswali yako ya kijinga. Unamuomba Mei Lee sio mimi. Nenda kamuukize mwenyewe.”

“Lakini we ndo umenishauri.“

“Kwahiyo?”

“Unatakiwa unielezee vizuri.”

“Sasa nikueleezee nini? Mimi sikufindishi jinsi ya kutengeneza ukaribu na mwanamke. Nashauri tu.” Akasema Maufeng na kuongozea. “Lakini sioni ugumu. Mfuate na umuombe mkatembee. Sio lazima iwe leo.”

“Ni ngumu sana.” akasema Mkuki.

“Basi unaweza ukaacha. Kwani ni lazima ujue kwanini anaficha sura?”

Akacheka kidogo Mkuki. “Mimi mwanaume. Najua ni vigumu lakini nitafanikiwa.” Akasema Mkuki na ikawa hivyo.

Jioni ya siku hiyo alimfuata Mei Lee nyuma ya nyumba ambapo alikuwepo huko akiimba. Huo ndio utaratibu wake kila jioni, kama si kwenda kuimba ufukweni basi hujichimbia nyuma ya nyumba, sehemu yenye bustani ndogo anayoitunza Mei Lee mwenyewe, na huko huupa moyo, roho na nafasi yake burudani tamu ya kujiimba nyimbo zake na za wasanii wengine anazozipenda.

Basi Mkuki alikwenda na kusimama nyuma ya pale alipokuwa ameketi Mei Lee; binti hakuwa akifahamu kuhusu ugeni huo, aliendelea kuimba kwa kujiachia kana kwamba alikuwa peke yake. Mkuki alimsikiliza hadi alipomaliza, kisha akafungua kinywa kumsemesha. “Unaimba vizuri sana.” Akazungumza huku akipiga makofi taratibu.

Mei Lee akageuka, akamuona Mkuki, akatazama chini kwa aibu.

“Unaimba vizuri mno.” Akasema tena Mkuki.

“Asante.” Akajibu Mei Lee kwa sauti ya chini sana ingawa Mkuki aliisikia.

“Unajua Mei Lee, wewe ni miongoni mwa waimbaji wachache duniani wenye sauti nzuri za asili. Hata nimeanza kupata wasiwasi juu ya ubinadamu wako, inawezekana wewe ni mmoja wa malaika watakaoipamba paradiso kwa nyimbo zao nzuri baada ya maisha ya dunia kufika ukomo.” akasema Mkuki huku akimsogelea Mei Lee.

Akaendelea.

“Natamani siku moja kila mtu athibitishe kwa sikio lake hiki ninachokwambia,” akamfikia. “Unaimba vizuri.” Akazidi kumpamba. Yote hiyo ilikuwa ni gia ya kumuingia, kutafuta jinsi ya atakavyompa zawadi lakini pia atakavyoomba kufahamua juu ya suala la uso na nywele.

Mei Lee alitazama chini muda wote, soni ilimtawala na hiyo ndiyo hulka yake; yeye ni msichana mwenye aibu kupita maelezo.

Mkuki akaketi pembeni ya pale alipokuwa ameketi Mei Lee, ilikuwa ni juu la benchi dogo lililotengenezwa katikati ya bustani ile nzuri iliyopandwa nyuma ya nyumba. Tena Mkuki alijitahidi kuwa jasiri wa aina yake kiasi kwamba asingeshindwa kuzungunza chochote kile kumwambia dada yake huyo—na hata walipokuwa wameketi walikuwa karibu karibu sana.

“Hatujawahi kukaa pamoja kama hivi,” akasema Mkuki; halikuwa swali lakini aliacha ukimya uchukue nafasi kana kwamba alikuwa akisuburi neno kutoka kwa mwenzie.

Alipoona kimya akaendeleahttp://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Inashangaza kiasi fulani. Unajua sisi ni ndugu sasa. Nadhani Tulitakiwa tuwe karibu tangu siku ya kwanza kufahamiana.” Akasema lakini bado mazungumzo yao yalionenkana ni ya upande mmoja. Mkuki akaamua kitu, akaamua kumshirikisha kwa mtindo wa kumuuliza maswali.

“Unapenda sana kuimba. Nani alikufundisha?”

“Kuimba?”

“Ndio. Nani aliyekufundisha kuimba.”

Mei Lee akajichekesha kidogo. “Mwenyewe tu.” Akajibu.

“Mwenyewe!?”

“Ndio.”

“Inawezekana vipi?”

“Sijui ni vipi inawezekana lakini imewezekana kwangu. Sijawahi kufundishwa na mtu yeyote. Niligundua tu kwamba muziki ni rafiki wa karibu zaidi ambaye naweza kumkabidhi maisha yangu na akanipa furaha muda wote.” Akajibu kwa kirefu na hiyo ni kwa sababu aliulizwa juu ya kitu anachokipenda.

Muziki ni kila kitu katika maisha ya Mei Lee, ni rafiki, mpenzi, nyumba ya amani, bahari ya furaha na mwenzi wa uhai wake. Ni rahisi kumnyima vyote na bado akajihisi binadamu, lakini si kumnyima fursa ya kuimba muziki. Na sauti yake ilikuwa ni kama kinubi, sauti tamu yenye uwezo wa kusimamisha mapigo ya moyo kwa kila mwenye nao, sauti ambayo kamwe huwezi kuisimulia kwa maandishi wala lugha ya picha isipokuwa tu kwa kuisikiliza mwenyewe kwa masikio yako; yaani hata kama wataalamu wa lugha wataamua kukaa chini kutafuta msamiati wa kuielezea sauti ya Mei Lee amini kwamba hawatafanikiwa kupata neno moja lenye kutosha kuidadavua.



**************************





“Hujawahi kutamani kuimba kwa ajili ya watu wengine?” Akauliza Mkuki.



Mei Lee akatulia kidogo kabla ya kujibu. “Natamani sana. Ndoto zangu ni kuwa mwanamuziki mkubwa, Thaiwan wote waifahamu sauti yangu ikiwezekana na dunia. Kuna jambo nataka kuueleza ulimwengu.”



“Jambo gani?” Akahoji Mkuki.





“Nataka dunia ifahamu kwamba Mungu wetu hajawahi kumuumba mtu kwa upungufu, hata tunaonekana ni wapungufu tumekamilika kiuumbaji.” Akasema.



“Upungufu kivipi?” Akauliza Mkuki, hakuwa ameelewa.



Mei Lee akamtazama kama mtu mwenye uhakika kuwa Mkuki alielewa alichokuwa anakizungumza, kisha akauliza kwa upole “Maufeng kakwambia nini kuhusu mimi?”



“Kuhusu wewe!?”



“Ndiyo.”



“Hapana. Maufeng ni swahiba wangu mno lakini hatujawahi kukuongelea. Kwani unafikiria nini?” Akajibu na kuuliza Mkuki.



Mei Lee akaonekanaa kutulia akimtazama Mkuki kwa makini kupitia uwazi mdogodogo uliotengenezwa na nywele zake zilizofunika uso.



“Unahisi nini? Hebu naomba nifafanulie unachotaka kusema. Nahisi kutokukuelewa kuanzia pale ulipozungumzia mapungufu ya binadamu.” Akahoji Mkuki.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Mei Lee bado alikuwa akimtazama tu; punde akaamua kufungua kinywa kuzungumza tena. “Unataka kujua nini kuhusu mimi?” Akauliza.



“Mimi?” Akauliza Mkuki, hakutarajia swali la aina hiyo kutoka kwa Mei Lee.



“Ndiyo wewe. Nambie, eleza kutoka moyoni.”



“Hakuna.”



“Hakuna? Kwahiyo huhitaji kufahamu chochote kuhusu mimi?” akauliza Mei Lee.



Mkuki akatulia kidogo akitafakari kisha baada ya sekunde tano akjibu.



“Nataka kufahamu... kuhusu... kwanini unafunika uso kwa nywele.” Akasema kwa kusuasua Mkuki.



“Ukishafahamu?” Akahoji Mei Lee, bila shaka alitarajia ombi lile kutoka kwa Mkuki.



“Kiu yangu itakatika.” Akajibu Mkuki.



“Vipi kuhusu mimi? Kiu yangu itakatika pia baada ya wewe kupata unachohitaji?”



“Wewe una kiu gani?”



“Nina kiu ya kuona watu wanaotamani kujua kwanini nafunika uso wangu kwa nywele hawaniachi baada ya kutimiza hitaji lao.”



“Una maana gani?”

Kabla ya kujibu Mei Lee akasimama, akasoegea mbele kidogo ya pale walipokuwa wameketi. “Wewe sio mtu wa kwnza kutaka kujua ni kwanini niko hivi, kwanini naficha uso wangu. Wengi waliotamani niliwaonesha, lakini hawakunipenda. Hawakutaka kuwa karibu na mimi.” akaeleza Mei Lee na kupiga kimya cha sekunde chache kisha akaendelea.



“Bado unataka kukata kiu yako?" Akauliza Mei Lee, hapa akigeuka na kumtazama Mkuki.



“Ndiyo.” Mkuki akajibu kwa kujiamini huku akitingisha kichwa kukubali,  na ndani akiwa ametutumisha shauku ya kutimiziwa hitaji lake hilo la muda mrefu.



Basi Mei Lee akauandaa moyo wake kwa ajili ya kutimiza hitaji la Mkuki; hawakuwa wamezoeana sana lakini kwa yale mazungumzo marefu waliyofanya alihisi ipo sababu ya kumuonesha. Alichokuwa akikificha hakikuwa kikimpendeza kama ambavyo aliamini kinawachukuza watu wengine. Ni watu kadhaa ambao walikuwa kama Mkuki, walitamani kujua ni kwanini anaficha uso wake kwa nywele lakini mara baada ya kufanikisha kufahamu hilo hawakutaka kuwa karibu naye tena.



Basi Mei Lee akajikweka sawa, akiwa ametazama chini akanyanyua mikono yake yote miwili hadi usoni, akazishika nywele zake na kuanza kuzitengenisha taratibu kwa kuzisogeza kushoto na kulia. Hadi kufikia hapo tayari mkuki alianza kuona kile alichokuwa anahitaji ingawa si kwa uwazi kama ambavyo angependa na hii ni kwa sababu Mei Lee alikuwa ametizama chini kwa aibu na fedheha.



Basi Mkuki akajipa ujasiri zaidi, akasimama na kumsogelea Mei Lee, akamshika kidevuni na kuuinua uso wake taratibu na papo hapo akaona kile kilichokuwa kikifichwa nyuma ya nywele na msichana huyo.

Ulikuwa ni uso wa ajabu sana, uso wenye tofauti kubwa mno, uso wenye kutisha usiokupa hamu ya kutaka kumtazama kwa muda mrefu. Uso wenye makunyanzi ya kama majeraha mabichi ya mtu aliyeungua moto; yaani unapomtazama ni kama yalikuwa yakitoa maji maji lakini haikuwa hivyo, uso wake ulikuwa ni mkavu tu, bali makunyazi yale yenye kukera yalionekana kama ‘donda bichi’.



Hali hii kwake aliitazama kama kasoro, ilimnyima amani, raha na fursa ya kufurahia zawadi ya uhai aliyopewa na Mungu. Alijichukia, alijitenga na watu pia kama ambavyo wengi walimtenga. Aliilisha nafsi yake imani ya kwamba hakuna mtu anayependa kumtazama na kweli alishiba upotofu huo na tangu hivyo alikuwa ni msichana mpweke.



Hakuzaliwa hivyo; hilo lilikuwa ni tatizo alilopita alipokuwa mtoto mdogo wa miaka sita. Aliugua ugonjwa wa ghafla, inasemekana ulisababishwa kwa kula samaki mwenye sumu. Alianza kuvimba mwili mzima mpaka usoni lakini matibabu ya hapa na pale yalimsaidia kiasi kwamba uvimbe katika  maeneo mengine ya mwili ulikata isipokuwa yale makunyanzi yaliyoharibu sura yake.



Hata Mkuki mwenyewe hakutamani kuendelea kumtazama lakini alijitahidi kutomkwepa kwa sababu hakutaka Mei Lee afahamu kuwa hata yeye ni miongoni mwa wengi wasiopendezwa na sura yake.



“Nina zawadi yako.” Akasema Mkuki kwa sauti ya taratibu, kisha akaingiza mkono kwenye mfuko wa suruali yake na kutoa ile cheni ya jedi aliyomnunulia, akamuonesha. Alifanya haraka namna hiyo ili kumtoa Mei Lee katika majonzi ambayo labda angepata kutokana na kile kilichokuwa kinaendelea kwa wakati ule.



“Umeipenda?” Akamuuliza, Mei Lee akajibu ndio kwa kutingusha kichwa.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Nikuvishe?” Akauliza tena na hata safari hii pia Mei Lee alijibu ndiyo kwa kutingishwa kichwa tu.



“Geuka.” Akasema Mkuki. Mei Lee akageuka taratibu na kumpa mgongo, naye akanyanyua mikono akiwa ameishika ile cheni, akamvisha taratibu na kuifunga.



“Tayari.” Akamwambia.



Hakika kitendo hicho kilimfanya Mei Lee ajione kuwa ni mwanamke aliyetimia; alijihisi ni kama malaika, kama dhahabu, kama almasi, kama malkia, kama kitu chenye thamani kubwa isiyosimulika. Hakuwahi kufanyiwa jambo la kiungwana kama lile na mtu yeyote duniani, zawadi ile na jinsi ilivyowasilishwa vikifanya amuone Mkuki ni mwanaume zaidi ya wanaume wote waliowahi kuumbwa na Mungu Mwenyezi.



Baada ya pale wakaketi kwenye benchi na mazungumzo yakaendelea hadi kuzama kabisa kwa jua.



*******************************



Tangu siku hiyo Mkuki na Mei Lee wakawa ni kama ndugu wa damu, kama chanda na pete, kama uji na mgonjwa, kama mapacha, kama roho na uhai. Siku ilikuwa ndefu kwa Mei Lee amkosapo Mkuki karibu; uwepo wake ulimfanya ajihisi raha na kwamba alikuwa na kila sababu ya kuishi duniani.



Jambo hilo lilihama hadi kwa mzee Wong, akajikuta anampenda sana Mkuki kwa sababu alikuwa ni mtu wa pakee aliyefanikiwa kumtoa Mei Lee ndani ya gereza la huzuni na sononeko.



Kwa utatu wao wakaunda familia moja bora sana, familia iliyosheheni upendo na amani kiasi kwamba hata kama Mkuki angaeomba kuondoka leo hii, mzee Wong na Mei Lee wasingekubali—alikuwa ni mwenzao, alikuwa ni mtu muhimu katika familia.



**********************************



Mkuki na Maufeng waliendeleza harakati za kujitafutia kipato kupitia uvuvi mdogo. Hata hivyo kipato chao kiliwawezesha kumudu mahitaji muhimu ya kila siku tu na si kufanya jambo lolote la maendeleo.



Hali hiyo ilimkwaza sana Mkuki na mara kadhaa hakuacha kuiweka wazi kwa rafiki yake Maufeng.



“Nafikiria tungetafuta biashara nyingine tukawa na chanzo kingine cha mapato mbali na uvuvi.” Alieleza Mkuki.



“Tunahitaji muda kufanyia kazi hilo.” Alijibu Maufeng.

Mwezi mmoja baadae tangu wazungumzie suala la chanzo mbadala cha mapato Maufeng alikuja na wazo. Alikuja na taarifa mpya ya jinsi ambavyo yeye na rafiki yake wataweza kufanikiwa kupata kipato zaidi.



“Kuna kisiwa kinaitwa Jiaju. Yaani huko kuna samaki balaa, na soko pia ni kubwa. Kuna meli zinatoka China na kuja kununua samaki hapo. Watu wameanza kukimbilia huko. Unaonaje tukienda.” Alieleza Maufeng Lau.



“Mtumbwi wetu unaweza kufika huko?” Mkuki akauliza.



“Hapana. Hauwezi. Ni mbali na hapa. Kwahiyo kama tutakubali kwenda inabidi twende na pesa ya kukodi mtumbwi huko. Yaani tunaweka kambi kabisa, kama ni wiki mbili au hata mwezi. Tutaangalia wenyewe.”  Akafafanua Maufeng.



Mkuki alivutiwa sana na taarifa ile na alishiwashika hasa kuhusu kwenda kwenye kisiwa hicho kidogo kiitwacho Jiaju kilichopo Magharibi mwa Thaiwan.



Hata hivyo kabla ya kwenda huko alihitaji ruhusa kutoka kwa baba yake mlezi; yaani mzee Wong. Alifikisha taarifa hiyo kwa mzee wake lakini alipata mrejesho wa tofauti na alivyotarajia.



“Hapana. Huwezi kwenda huko.” Yalimtoka mzee Wong.



“Kwanini? Naenda halafu nitarudi, naenda kwa sababu ya kutafuta pesa zaidi.” Akajitetea Mkuki.



“Unapajua Jiaju?” Akauliza mzee Wong na kuendelea kabla hata ya Mkuki kumjibu. “Ni ardhi ambayo hakuna mzazi anayeweza kumruhusu mwanaye kwenda huko hata kama atapata ujira wa amali zote za dunia. Kule ni kuzimu.” Akasema mzee Wong.



Kisiwa cha Jiaju kilipatikana Magharibi mwa Thaiwan. Kilikuwa ni kisiwa kidogo ambacho kinaitenganisha nchi hiyo pamoja na China, lakini ilikuwa ni rahisi kufika Jiaju ukitokea Thaiwan kuliko kutokea China.



Huko kulikuwa na eneo la bahari ambalo walipatikana samaki wengi mno; na wavuvi wengi hasa kutoka Thaiwan walipakimbilia. Mbali na kuwa na samaki wengi, Jiaju pia ilikiwa na soko kubwa la samaki. kampuni nyingi kubwa hasa kutoka China zilinunua samaki kwa wavuvi wadogo waliopo huko na walisafiriaha samaki hao kwa kutumia boti zao. Soko hilo la samaki lilikifanya kisiwa cha Jiaju kuwa moto, kilikuwa ni kisiwa kidogo lakini chenye muongiliano mkubwa wa watu nakufanya iwe ni sehemu changamfu. Hata hivyo huko hakukuwa na makazi ya watu; Jiaju ilikuwa na mazingira ya kama maeneo mengi ya mgodi; yaani baa, vilabu vya pombe, nyumba za kulala wageni na madanguro yalikuwa lukuki.



Biashara chafu kama ukahaba ilifanyika huko, uuazaji wa mihadarati kwa ajili ya matumizi ya kawaida na pombe ndiyo ilikuwa habari ya Jiaju—hivyo kutokana na yote hayo suala kama ugonvi wa mara kwa mara na hata kuuana yakikuwa ni matukio ya kawaida ingawa napo palikuwa na kituo cha polisi.



“Msimamo wangu ni kwamba hauwezi kwenda. Naomba mjadala kuhusu Jiaju uishie hapa.” Alisema mzee Wong  huku akionekana kumaanisha kilitchotoka kinywani  mwake, alikuwa akimchukilia Mkuki kama mwanaye wa damu hivyo hakuwa tayari kuona akiangamia kwa namna yoyote ile.



Basi Mkuki hakuwa na budi kumsikiliza mzee wake, mwenyeji wake. Alichokifanya ni kumtafuta Maufeng na kumueleza ukweli. Hata hivyo Maufeng alionekana ni mwenye kiu, hivyo hakutaka kukubali kirahisi namna hiyo juu ya kile ambacho Mkuki alielezwa  na mzee Wong; akashauri kitu.

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Kule kuna ela Mkuki. Na huu ndo umri wetu wakuzifuata. Usipende sana kusikiliza maneno ya wazee, wao wapo kwa ajili ya kutuvunja moyo kwa sababu ni waoga, na uoga wao ndio umesababisha wazeeke maskini. Twende hata bila kuaga, tukirudi na pesa hakuna atakayezikataa eti kwa sababu tilitoroka, wote watatupongeza na kutuona mashujaa.”



“Tutoroke!?”



“Ndiyo. Sasa unadhani tutafanya nini kama si hivyo?”





**********************************



ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog