Search This Blog

Thursday 27 October 2022

ANGA LA WASHENZI (1) - 2

 











    Simulizi : Anga La Washenzi (1)

    Sehemu Ya Pili (2)







    Alikuwa amevalia suruali pana ya malighafi laini, kaushi nyeusi pasipo sidiria, miguuni akiwa peku. Nywele zake zilikuwa timu, kinyumbaninyumbani. Nyuma ya kiuno alikuwa amechomeka bunduki ndogo.



    Japokuwa alishangazwa na Jona kujua makazi yake, ila hakuwa na wasiwasi sana. ni ‘mchora picha tu, alijiambia moyoni akisogelea mlango.



    “Karibu.”



    Jona akazama ndani pasipo kusema lolote. Akaketi na kukunja nne. Miranda naye akafuatia nyuma, akaketi kwenye kiti kilichowafanya watizamane vema.



    “Najua ujio wangu umekustaajabisha, pengine ulitegemea nisingekuwa hai wakati huu ama basi ni mlemavu, samahani sana,” alisema Jona kwa kujiamini. Miranda akakunja ndita za kukanganyikwa.



    Hakupewa muda wa kuuliza, Jona aliendelea kuongea.



    “ … Anyway, I am tired of your bullshit. Mnataka nini kwangu? Ile picha? Ni picha ndiyo inawafanya mtake kunitoa roho? Mmeona picha haitoshi sasa mnawinda roho yangu?”



    “Jona, please calm down. Sielewi unachokizungumza. Nani anataka kukutoa roho? Embu twende taratibu taratibu, umepajuaje hapa?”



    Jona akatabasamu.



    “Usitegemee kama nitajibu swali lolote toka kwako. Sijaja hapa kufanyiwa mahojiano bali kutoa tamko na angalizo. Mosi, hamtapata picha yoyote toka kwangu. Pili, acheni mara moja kunifuatilia, la sivyo …” Hakumalizia, ila macho yake yalisema kila kitu.



    Akanyanyuka na kuondoka zake akimwacha Miranda kwenye bumbuwazi.



    Mwanamke huyo akamtazama Jona akifungua mlango wa geti na kuufunga kwa kuubamiza. Akagundua mlinzi hayupo. Haraka akanyanyuka na kwenda kutazama.



    Akamkuta mlinzi akiwa hana fahamu.



    Akampigia simu Kinoo na kumtaka aje nyumbani upesi. Baada ya muda mfupi Kinoo akatia miguu yake eneoni akitumia Range Rover sport nyeupe. Alikuwa amevalia ‘ki body’ cheusi na suruali ya jeans aliyoifunga na mkanda kiunoni, miguuni akila moka nyeusi.



    Miranda akamweleza yale yote yaliyotukia kuhusu Jona.



    “Si unaona sasa?” Kinoo akatahamaki. “Mi’ ndo’ mana n’likuambia tummalize tu, we ukawa unavunga vunga. Ona sasa!”



    “Kinoo, embu uwe unatumia akili hata mara moja moja. Yani we umeona hilo ndo’ la kukimbilia kuropoka?”



    “Haya, we endelea kun’zarau.”



    “Si kwamba nakudharau, nakwambia ukweli. Kuna maswali ya kuanza kujiuliza na kuyatafutia majibu, na si kuanza kurusha risasi za lawama.”



    Kinoo akashusha pumzi ndefu puani na kubinua mdomo wake.



    “Haya sema nakus’kiza.”



    “Kinoo, huyu mchora picha si tu mchora picha. Nimeshangazwa kwa namna alivyopajua hapa na hata kujiamini kwake.



    Kama haitoshi, namna alivyomkabili mlinzi, kunazidi kunifanya nihofie. Pengine mtu huyu anahitaji jicho la pili, ni mtu mwenye ujuzi binafsi ama mafunzo.



    Zaidi ya hapo, kwa necha ya maongezi yake kuna watu wanamfuatilia, na hawa watu wanataka kumuua japo hajaweka wazi ni wakina nani na wametumia njia gani. Ila wapo, na ajabu sio sisi! Kwani kwa muda kidogo hatujasumbuka naye, na hatujawahi pia kutishia uhai wake.



    Unadhani nini kinaendelea? Ina maana mchora picha huyu naye anataka kumalizwa kama Bite?”



    Kinoo akaguna na kubinua lips zake nyeusi.



    “Hilo halina shaka. Ina maana tayari wanajua kuhusu mchora picha huyu, na sasa wanataka wamalize ushahidi kabisa kisibakie hata punje. Hii ina maana wanajua kulikuwa kuna mahusiano kati ya Bite na huyu mchora picha.”



    “Ndiyo maana yake. Na naona msisitizo ni kumuua mchora picha kuliko kuipata picha yenyewe. Wanataka kummaliza. Ina maana kilichomo kwenye picha hawakihitaji, wanakijua?”



    Kinoo akapandisha mabega juu.



    “Leo inabidi tupate picha hiyo, Kinoo,” Miranda akasema kwa msisitizo. “Tusipoipata leo, kuna hatihati tukaikosa daima.”





    **





    Wakati huo upande huu ukiwa unateta, upande mwingine kwenye laini mojawapo ya simu maongezi ya Nade na mheshimiwa waziri, Eliakimu Mtaja, nayo yakawa yanachukua nafasi.



    Nade alikuwa amejikobeka mahali fulani alipoegemea ukuta.



    Kumbe alikuwa ndiye mwanamke yule Jona aliyemuona kule Kariakoo. Nguoze zilisema hivyo.



    Eneo hili alilokuwepo halikujulikana kwa urahisi.



    “Nimemshuhudia kwa macho yangu akiingia na kutoka kwa Miranda.”



    “Una uhakika?”



    “Ndio, mheshimiwa.”



    “Ina maana wanajuana na Miranda?”



    “Itakuwa wanajuana. Hakukaa kwa muda mrefu ndani.”



    “Watakuwa wanafanya ishu gani na Miranda?”



    “Sijajua mkuu. Sijajua pia nani aliyejaribu kumuua kwa kumgonga na gari. Inaonekana kuna mambo kadhaa tusiyoyafahamu kuhusu Jona.”





    “Mfuatilie kila nyendo,” mheshimiwa akanguruma. “Hakikisha kama anayoyafanya yanahusiana na Mariam, kama ndiyo unipashe habari upesi. Kama sio basi fanya ujue ni jambo gani.”



    “Sawa, mkuu,” Nade akajibu na kukata simu.







    ***







    “He’s promised, so very soon things gonna be ok,” (Ameahidi, kwahiyo karibuni vitu vitakuwa sawa) Miranda alisema kwa sura ya uhakika. Alikuwa anaongea na mwanaume mzungu, makadirio ya miaka hamsini na mambo hivi, mwenye ndevu nyeupe zilizochongwa vema, na nywele za wastani kichwani.



    Mwanaume huyu alikuwa amevalia shati jeupe lililoziba mikono yake, suruali nyeusi na moka rangi ya kahawia, iking’aa mithili ya kioo. Shingoni alikuwa amejinyonga na tai rangi ya chinikiwiti.



    Mkono wake wa kushoto alikuwa ameuvika saa kubwa rangi ya dhahabu, huku mkono wake wa kuume ukiwa umekamatia sigara kubwa ya kaki iliyokuwa inafuka kama gari moshi.



    Mkono huu ulikuwa na kazi mbili, moja kupeleka sigara mdomoni, na pili kukung’utia sigara kwenye kisosi kilichokuwapo mezani.



    Miranda alikuwa amevalia gauni jeusi linalombana na kumsadifu umbo. Nywele zake zilikuwa zimetengenezwa na kuundwa vema kama nyasi za msonge. Shingoni alikuwa na mkufu wa dhahabu, masikioni hereni za ghali.



    Mezani alikuwa ameweka pochi yake ndogo nyekundu yenye zipu kubwa. Alikuwa ananukia kana kwamba ametoka kuoga kwenyee dimbwi la marashi ya Uajemi.



    Waliendana na makazi waliyopo – nyumba kubwa ya kisasa iliyozungukwa na bustani ya majani na maua. Mlinzi getini mwenye bunduki na mbwa mkubwa mchanganyiko wa mbegu za Ulaya.



    Lakini kwa mujibu wa mavazi yao, usingekosea kubashiri kuwa watu hawa wana safari muda si mrefu ya kwenda mahali fulani. Tena penye taadhima. Haingii akilini kusema wamejikobeka vile kwa ajili ya makutano tu.



    Mwanaume huyu mzungu anafahamika kwa jina la Brown Curtis, Ama kwa kifupi BC kama watu wake wa karibu na yeye pia anavyopenda kuitwa. Sauti yake ni nyembamba na ya chini, macho yake ni makali rangi ya bluu.



    “But his price goes higher every now and then. It becomes very expensive to afford him,” (Lakini bei yake hupanda kila sasa na baadae. Inakuwa gharama kubwa kummudu,” alisema BC kabla hajapeleka sigara mdomoni na kuinyonya mithili ya mtoto anyonyavyo titi la mama yake.



    "But we have no choice. We depend on him so much. Or have you got someone else?" (Lakini hatuna chaguo. Tunamtegemea mno. Au umeshampata mtu mwingine?" Miranda aliuliza.



    BC akatikisa kichwa.



    "No! And that's the real problem. I must find a way out." (Hapana! Na hilo ndilo tatizo haswa. Ni lazima nitafute namna.)



    "Be keen. He knows most of our moves, he may spoil the car if we deny him the fare." (Kuwa makini. Anajua harakati zetu nyingi, anaweza kuharibu gari akijua tumemnyima nauli.)



    "Don't worry, I will be the first one to take action after getting an exit door. He cannot do anything stupid unless I am dead," (Usijali, nitakuwa wa kwanza kufanya jambo nikishapata mlango wa kutokea. Hawezi akafanya jambo lolote la kijinga labda niwe mfu,) alisema BC uso wake ukiwa umezibwa na moshi wa sigara



    Mara akatokea dada wa kazi. Alikuwa amevalia sare rangi nyeusi na nyeupe akibebelea trey yenye glasi kubwa ya sharubati ya Strawberry.



    Akaitua mezani na kumkaribisha Miranda, kisha akaenda zake.



    "Any suggestion?" (Wazo lolote?) BC aliuliza akimtazama Miranda. Alijua mwanamke huyo hatokosa cha kusema.



    Miranda akapandisha mabega juu.



    "It's just ok if you believe things won't go out of your hands." (Ni sawa tu kama unaamini vitu vitakuwa poa.)



    "Yes. We gat to do something, he takes almost half of the profit. It is dangerous ... let us see what will happen." (Ndio. Inabidi tufanye kitu, anachukua karibia nusu ya faida. Ni hatari ... acha tuone nini kitatokea.)



    Kukawa kimya kidogo. BC alikuwa anavuta pafu za sigara, Miranda akipiga mafundo ya sharubati yake tamu.



    "What about the report I sent? Have you gone through it?" (Vipi kuhusu ripoti niliyokutumia, umeipitia?) Miranda alivunja ukimya. BC akakohoa kwanza mara moja kabla hajajibu.



    "I have done so. It's already sent ... and thanks for reminding me, the results are nothing but perfect! You can’t imagine even some governments have already booked them secretly." (Nimeipitia. Tayari imeshatumwa ... na shukrani kwa kunikumbusha, matokeo ni mazuri sana! Huwezi amini hadi baadhi ya serikali wameshaweka oda zao kwa siri.)



    "That's nice! Then we have to produce more!" (Hilo ni jema! Basi inabidi tuzalishe zaidi!)



    "Exactly, men are in the laboratories, as we are talking, working day and night. In fact more of it will be here soon special for our enemies." (Kabisa, watu wapo maabara, hapa tunavyoongea, wakifanya kazi usiku na mchana. Vile vile itatumwa hapa zaidi kwa ajili ya maadui zetu.)



    "It's better! Enemies now are closer than before." (Ni bora! Maadui sasa wapo karibu kuliko awali.)



    "All for the sake of business! Competition is stiff. Chemical and biological weapons are marketable for its effectiveness though they are prohibited in most places. I think it’s time now to put emphasis on this." (Yote kwasababu ya biashara! Ushindani ni mkubwa. Silaha za kemikali na baiolojia zina soko kwasababu ya ufanisi wake japo zinakatazwa mahali pengi. Nadhani ni muda sasa wa kuweka msisitizo kwenye hili.)



    BC alitazama saa yake ya mkononi, kisha akamwambia Miranda.



    "It's time. Let's go!" (Muda huu. Tuondoke.)



    Miranda akamalizia kinywaji chake, BC akaminyia sigara yake kwenye kisosi kuizima. Wakanyanyuka na kwenda kwenye gari, Jeep nyeusi aina ya Cherokee. Wakakwea na kutoka ndani ya jengo.



    Mwanaume ndiye alikuwa akiendesha, mwanamke akiwa amekaa pembezoni yake.



    Walipoacha tu geti kwa umbali mdogo, Miranda akatoa simu yake kwenye pochi na kumtumia ujumbe Kinoo:



    “Naweza nikakawia. Hakikisha unapata ile picha leo hii kama tulivyokubaliana.”



    Ujumbe ulipofika, akarejesha simu yake ndani ya pochi.



    “I don’t have to tell you about this, you know how important it is. We have to expand our network tonight. We must look for another hand. You are an expert in that and that’s why I go with you.” (Sina haja ya kukuambia kuhusu hili, unajua namna gani lilivyo muhimu. Inabidi tutanue mtandao wetu. Ni lazima tutafute mkono mwingine. Wewe ni mtaalamu kwenye hilo na ndiyo maana naenda nawe.)



    “I will do my best,” (Nitajitahidi,) Miranda akasema kwa ufupi, kukawa kimya.





    ***







    “Naomba maji makubwa ya Kilimanjaro, ya moto. Na waambie jikoni waniandalie ndizi tano na nyama rosti,” Jona alitoa oda kwa mhudumu. Mhudumu akatikisa kichwa chake na kwenda.



    Mwanaume huyu alikuwa ndani ya bar akatizayo kabla ya kwenda nyumbani kwake. Majira yalikuwa ya giza sasa. Alikuwa amechoshwa na uchovu, na mgongo wake ulikuwa unamuuma kwa mbali kutokana na purukushani ile ya ajali.



    Akiwa anangojea huduma, akatoa simu yake na kuiangaza. Hakukuwa na ujumbe wala missed call. Akatahamaki Mheshimiwa hajamtafuta mpaka muda ule.



    “Hajaona missed calls zangu?”



    Alikumbuka maagizo ya Mheshimiwa kwamba akiwa amebanwa basi amtafute Nade na kumwambia shida yake, ila hakutaka kufanya hivyo, akaamua kuachana na jambo hilo.



    Kulikuwa kuna jumbe kadhaa toka Facebook ila hakutaka kusumbuka nazo, akazipuuza.



    Alipoweka simu yake mezani, macho yake yakatekwa kumtazama mwanaume fulani aliyekuwa anaingia ndani ya eneo ya bar. Mwanaume huyu alikuwa amevaa suti nyeusi na tai nyekundu.



    Aliketi karibia na eneo kubwa la kutokea.



    Alikuwa ni Bigo! Mwanaume aliyeagizwa kummaliza Jona.



    Jona alimtazama mwanaume huyu kwa muda kidogo. Atensheni yake ikaja kuharibiwa na mhudumu akileta maji makubwa aliyoagizwa, akayapokea na kumiminia kiasi ndani ya glasi.



    Mhudumu akamfuata Bigo, mwanaume huyo naye akaagiza maji makubwa kama yale ya Jona. Mhudumu akamskiza na kwenda zake.



    Mara tatu Jona akakutana macho kwa macho na Bigo. Alikunywa glasi mbili za maji kisha akanyanyuka kabla hajakutana na mhudumu akimletea chakula chake alichoagiza jikoni.



    “Kiweke tu hapa mezani, naenda maliwato nakuja,” alisema Jona, kisha akaenda uani kwa ajili ya haja ndogo.



    Bigo alitaka kumfuata ila akasita. Hakuwa analijua eneo hilo vizuri, ilimradi alikuwa na uhakika kwamba Jona atarudi kwasababu ameacha mizigo yake mezani, basi akatuama asiwe na mashaka.



    “Acha nikamuulie kwake,” alisemea kifuani, akaendelea kunywa maji yake taratibu.



    Upande wa pili Jona akamaliza haja yake, akafunga zipu ya suruali na kuanza safari ya kurudi alipokuwepo.



    Lakini kabla hajamaliza safari yake, hatua chache tu toka chooni, macho yake yakaona gari Mark 2 nyeusi kwenye kauwanja kadogo ka maegesho ya magari hapo bar. Haraka kumbukumbu yake ikamjuza gari hilo ndilo lile lililotaka kumgonga.



    Akataka kuhakikisha.



    Kwa tahadhari akalisogelea na kulitazama mbele juu ya bodi, akaona limebonyea. Akaligusa kwa nyuma na mgongo wa kiganja, kama haitoshi akainama na kusogeza kichwa chake uvunguni mwa gari.



    Akagundua gari hilo lilikuwa limefika hapo muda si mrefu. Nani ameingia bar muda si mrefu? Hakuna mwingine mbali na mwanaume yule aliyevalia suti, akili yake ikampa majibu haraka.



    Basi akajikuta akitabasamu.



    “Naona amenifuata kumaliza kazi yake,” alisema kisha akajirudisha kwenye kiti chake. Akaketi na kumtazama Bigo.



    Alikunywa maji yake taratibu akiyapanga mambo kichwani. Alipomaliza akamuita mhudumu na kumlipa pesa yake kisha akanyanyuka na kubeba vitu vyake. Taratibu akashika njia ya kwenda nyumbani.



    Alitumia njia tofauti na ile kuu. Kadiri alivyokuwa anasonga mbele, basi akawa anaongeza ukubwa wa hatua zake.



    Haikupita muda mrefu, akahisi kuna gari linakuja nyuma yake. Pasipo kutazama akajua ni lile Mark 2. Kwa mwendo wake wa ukakamavu akaendelea kukata mbuga. Ndani ya muda mfupi, mbele ya nyumba yake.



    Akafungua geti na kuzama ndani.



    Hili lilikuwa kosa la kwanza Bigo kulifanya – kumruhusu Jona azame ndani ya nyumba. Hakujua kama amefanya kosa. Alimchukulia Jona kama mchora picha tu. Kwa akili yake akaona Jona amejiingiza kwenye kaburi lake.



    Somo la namna mwanaume mwanaume huyo alivyokwepa ajali halikumuingia akilini, au pengine hakulielewa.



    Alishuka akaliacha gari ‘on’ kwa minajili kwamba atarejea muda si mrefu na kuhepa zake baada ya tukio. Mkononi alikuwa amebebelea bunduki ndogo, na tayari uso wake ulikuwa umevikwa kinyago cheusi.



    Kinyago chenye sura ya fuvu la kichwa cha binadamu.



    Akazama ndani kwa kuruka ukuta kama kima. Taratibu akausogelea mlango, akajaribu kuusukuma, ulikuwa umefungwa. Basi hakutaka kuzozana nao kwasababu alitaka mambo yawe kimya kimya.



    Alitaka amalize kula pasipo kujaza nzi.



    Akazunguka jengo kupitia madirishani, kwa malengo auendee mlango wa uani nao aujaribu, pia amuone Jona yupo pande gani ya nyumba.



    Alijuta kwanini hakubebelea kiwamba cha kumezea sauti ya bunduki. Lakini akatafuta ahueni ya juto hilo kwa kujitia hana haja ya kutumia hiyo silaha.



    “Nitatumia mikono yangu tu,” akajisemea kifuani. “Huyu si wa kupoteza risasi yangu.”



    Akazunguka dirisha la kwanza, hakuona kitu. Dirisha la pili na la tatu pia. Akiwa anasogelea la nne, ambalo ndilo lilikuwa la chumbani kwa Jona, akasikia sauti ya kitu kama karatasi nyuma yake.



    Haraka akageuza shingo kutazama. Hakumuona mtu! Akaendelea zake kufuata dirisha, akarusha macho ndani. Hakuona mtu.



    Sasa alikuwa karibu na mlango wa uani. Kama hatua tano hivi aukute.



    Alipiga hatua tatu, akahisi tena sauti ile ya mwanzoni. Haraka akageuka, saa hii akinyooshea mdomo wa bunduki huko. Hakuona mtu! Aliporejesha uso wake mbele, akakutana na mwanaume amesimama.



    Alikuwa Jona.



    Kabla hata kichwa cha Bigo hakijajua nini la kufanya, akashangaa kuona Jona yupo juu, kufumba na kufumbua, akala teke lenye kilo nzito lililomtupa chini kama fuko la saruji!



    Akanyanyuka upesi kwa kujifyatua na mikono yake. Ila Jona hakumpatia mwanya hata kidogo, akachumpa na kujilaza hewani akijizungusha kama tairi. Akachanua miguu kumzawadia tena teke.



    Mara hii Bigo akaliona, akainama kukwepa, kunyanyuka, hajakaa sawa, mkono wenye bunduki ukapigwa, bunduki ikarukia mbali.



    Jona akatabasamu. Akatanua miguu yake na kumuita Bigo kwa ishara. Sasa Bigo akajua anapambana na mtu, mwanaume, sio ‘mchora picha’.



    Alikuwa ameingia peku kwenye kiwanja chenye mbigiri. Na sasa hakuwa na budi zaidi ya kuonyesha uanaume wake.



    Alikunja ngumi akajongea kwa kasi. Akatumikisha kiuno chake kurusha mateke mazito, mateke yakapita kando ya kichwa cha Jona. Akapeleka ngumize, akarudisha viwiko, navyo vikanyimwa mwelekeo.



    Baada ya dakika moja, rasmi Jona akaanza kujibu mashambulizi akiwa tayari ameshamsoma adui yake ndani ya muda huo mfupi.



    Hakupoteza nguvu, akapiga maeneo dhoofu kwenye mwili wa binaadamu, ambazo kitaalamu kwenye mchezo wa mapigano, martial arts, huitwa pressure points.



    Ncha za ngumi yake zilitafuta kingo za kwapa za Bigo, akatia ganzi mikono ya adui. Akampiga pia chini kidogo, katikati ya shingo, penye kashimo kanachotenganisha shingo na kifua, na kummalizia juu ya kitovu kwa hatua moja moja na robo ya vidole.



    Bigo akawa hoi.



    Jona akamvua kinyago na kumpeleka ndani sebuleni, akamfunga kamba kwenye kiti kisha akachukua kiti kingine na kukisogeza karibu. Akachukua na chupa kubwa ya mvinyo na glasi yake, akamiminia kinywaji humo na kupiga fundo moja akiketi.



    “Habari yako? – hatukuwa tumesalimiana,” alisema Jona akimtazama Bigo.



    Bigo hakusema kitu. Jicho lake la kushoto lilikuwa jekundu mno. Na kushoto kidogo mwa jicho hilo kulikuwa kuna mfereji mdogo wa damu ukitokea kwenye jeraha la kiasi.



    “Haya,” Jona akapandisha mabega yake juu. “Sitajali kama hutaki salamu yangu. Vipi na kinywaji nacho? Hutaki?”



    Bigo akaguna kama mtu anayetaka kuangua kicheko. Akasema:



    “Siku zako zinahesabika, msanii. Utaenda kuonja udongo muda si mrefu.”



    Jona akatabasamu. Akanywa kwanza mafundo matatu ya kinywaji chake.



    “Inaonekana unaona kinyume, ndugu yangu. Kwa unavyoona, kati yangu na wewe nani anaenda kuonja udongo muda si mrefu?”



    Bigo akaguna kwa kiburi.



    “Anyway, sina muda mwingi hapa,” Jona akasema akitazama saa yake ya mkononi.

    “Muda si mrefu itanibidi nipumzike kwa ajili ya kesho, nina kazi za kufanya na watu wa kuwaona. Hivyo basi ningependa kwenda moja kwa moja.



    Wewe ni nani? Na umetumwa na nani?”



    Kimya.



    “Najua itakuwa ngumu kwako kusema, ila nisingependa tukaumizana na kutiana ukilema alafu ndiyo useme, so tuokoe muda.”



    “Okoa muda wako kwa kuniua, msanii,” Bigo akasema, kisha akatabasamu.



    Jona akanywa mafundo mawili kwa staili ya tarumbeta kisha akanyanyuka na kumsachi Bigo, akamchomoa funguo za gari.



    “Unaenda wapi?” Bigo akawahi kuuliza.



    Jona akamtazama na kumpuuza kisha akaenda zake nje mpaka kwenye gari la Bigo. Akafungua mlango na kuanza kupekua chombo hicho akitazama huku na huko huku akisaidiwa na kurunzi.



    Akapata simu mbili, risasi nne, leseni na picha nne aina ya pasipoti. Akarejea ndani.



    Akaviweka vitu alivyovipata juu ya meza alafu taratibu akaanza kukipitia kimoja baada ya kimoja.



    “So unaitwa Alfonce Bigo,” alisema Jona akitazama leseni. Bigo alikuwa kimya akimtazama kwa macho makali, mdomo ameupinda.



    Alimaliza kutazama leseni akaiweka juu ya meza, akatazama pasipoti zile nne: zilikuwa za watu tofauti tofauti.



    “Na hawa nao umepanga kuwaua ama?”

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Achana na vitu vyangu, havikuhusu!” Bigo akafoka. Jona asimjali, akaendelea na kazi yake.



    Aligeuza pasipoti akazitazama kwa nyuma, akaona zimeandikwa kwa mbali maneno ya kichina. Kila pasipoti ilikuwa na maneno hayo.



    Aliziweka kando akateka simu na kuanza kuzikagua. Moja ilikuwa ni smart phone, Nokia Lumia kubwa nyeusi, nyingine ikiwa ndogo ya kawaida, tekno, nayo nyeusi kwa rangi.



    Simu zote zilikuwa zimefungwa kwa namba. Mtu kuingia na kutazama ilikuwa ni mpaka atie namba sahihi.



    Bigo alijua Jona hataweza kufungua simu hizo, kwahiyo hapa akawa na amani na taarifa zake zilizomo ndani, zipo salama.



    Alitegemea muda si mrefu Jona atamuuliza kuhusu hizo namba. Na aliapa kutozisema hata iweje, atazilinda kwa uhai wake.



    Kinyume na matarajio, Jona hakumuuliza chochote, bali akanyanyuka na kwenda chumbani alipotoka na tarakilishi mpakato nyeusi aina ya HP, na waya wa kuhamisha data, USB.



    Akaweka tarakilishi mezani na kuiwasha kisha akachomeka waya wa kuhamisha data toka kwenye simu kwenda kwenye tarakilishi.



    Sasa hapo akawa huru kufikia mafaili yaliyopo kwenye simu ya Bigo pasipo kutia namba zozote. Mafaili yote akawa anayaona kwenye kioo cha tarakilishi yake.



    “Wewe mshenzi acha kupekua simu yangu!’ Bigo aliwaka akitikisa mwili wake kwanguvu. Alitaka kujichopoa toka kwenye kamba. Alijitahidi sana kujing’amua lakini akaishia kupata tu maumivu.



    Hakufanikiwa.



    Jona, kana kwamba hasikii kelele za Bigo, akaendelea kuperuzi mafaili ya simu. Kuokoa muda akayakopi mafaili hayo na kuyahamishia kwenye tarakilishi yake kwa malengo ya kuyapitia atakapopata muda.



    Alipomaliza akachomoa waya, akatoka mezani na kumjongea Bigo.





    ***





    Nje ya nyumba ya Jona kulikua tulivu. Watu walikuwa ndani ya majengo yao na familia zao. Mataa yalikuwa yanamulika, na kelele pekee zilizokuwa zinasikika ni za watoto wakicheka ndani ya uzio.



    Kama ungelipita hapo, basi usingeliwaza kama kuna tukio linaendelea ndani ya nyumba ya Jona, japokuwa ndiyo nyumba pekee iliyokuwa imepaki gari kwa nje.



    Ndani ya muda mfupi, linatokea gari lingine. Kwa mbali halionekani kutokana na mwanga mkali wa taa. Linaposogea karibu na kufifisha taa, laonekana vema – ni Range Rover sport nyeupe.



    Ndaniye alikuwamo bwana Kinoo peke yake. Akalipaki gari nyuma ya Mark 2, kisha akashuka.



    Kama kawaida, alikuwa amevalia ‘kibody’ cheusi kilichobana kifua chake kipana pamoja na suruali ya jeans na moka nyeusi kwa chini.



    Aliitazama Mark 2 kwa muda kidogo akijiuliza ni la nani. Akarusha macho yake ndani ya jengo la Jona, hakuona kitu.



    “Ana mgeni au?”



    Akalikagua gari lile Mark 2 kabla hajazama ndani kwa kuruka ukuta baada ya kuona mlango umefungwa. Naye mkononi alikuwa amebebelea bunduki ndogo, na mwendo wake ulikuwa wa tahadhari.



    Angalau huyu alikuwa amepewa angalizo na Miranda juu ya Jona.



    Alisogelea dirisha la sebule, akachungulia ndani. Hakumuona Jona, ila akamuona mwanaume aliyeketishwa kwenye kiti na kufungwa kamba. Hakumtambua mwanaume huyo kwani alikuwa amezibwa na kinyago usoni.



    Lakini kinyago hicho kikamgutua. Kilikuwa ni cheusi chenye umbo la fuvu la binadamu. Alikumbuka Miranda aliwahi kumwambia kukihusu. Ya kwamba mwanaume yule aliyemvamia kuchukua kamera, alikuwa amekivaa.



    Ina maana ndo’ huyu? Akajiuliza. Anafanya nini hapa akiwa amefungwa kamba?



    Sasa kidogo Kinoo akaanza kuelewa kwanini Miranda alimwambia 'mchoraji' yule, ambaye ni Jona, hakuwa mchoraji tu, ni mtu mwenye ngebe za mafunzo na ujuzi.

    Hakutaka kuingia ndani haraka bali ausome kwanza mchezo, Jona yupo wapi? Na anamfanya nini huyu mtu aliyeonekana dhahiri kuwa mateka?

    Akatulia kungoja. Kwa dakika kama nne pasipo kuona wala kusikia jambo la kulituhumu.

    Alikuja kushtuka aliposikia chuma cha baridi kisogoni mwake, na sauti ya Jona ikamuamuru:

    "Tulia hivyo hivyo! - mikono juu!"

    Akatii amri. Kwa uzoefu wake alishajua ni mdomo wa bunduki ndiyo ambao upo kisogoni. Ila alikuwa mkaidi kuwa mpole kirahisi.

    Akaanza kufikiri ni njia gani inaweza kumuokoa akaushika mchezo.

    Ila kama vile alishtukiwa, akaonywa:

    "Ukijitia mjanja, nakutoboa kichwa!"

    Akatulia tuli, macho yake yakiangaza angaza kana kwamba mtu mwenye haraka atafutaye ufunguo wa gari.

    "Haya ongoza ndani!" Jona akaamuru. Pasipo kubisha, Kinoo akaanza kuchukua hatua kusogelea mlangoni.

    Kichwani mwake alitafakari ilikuwaje akadakwa kirahisi hivyo? Alijiona mjinga na mzembe pia.

    Endapo asipofanikisha hili, Miranda ataenda kumlaumu sana. Kumtusi na kumshusha vyeo.

    Hivyo lazima apate namna.

    Alipokaribia mlangoni, upesi akakisogeza kichwa chake kukwepa mdomo wa bunduki kabla Jona hajafanya lolote.

    Kisha akautwaa mkono wa Jona na kujaribu kuupoka silaha.

    Wakavutana huku na huko nguvu zikitumika. Kinoo akamzidi nguvu Jona, akaiteka silaha akimsukumizia kando mpinzani wake.

    Ila kabla hajafanya kitu na bunduki hiyo, Jona akautuma mguu wake, haraka sana, kuutengua mkono wa kulia wa Kinoo uliobebelea bunduki.

    Bunduki ikaangukia chini!

    Wote wakaitazama kwa macho ya ashki ila wasithubutu kuinamisha migongo yao kwa kumhofia mwenziwe.

    Kuinama kunamaanisha kumpa fursa adui akutende atakavyo, hilo kosa hakuna aliyetaka kulifanya.

    Wakaachana na bunduki wakitazamana kama mafahari ya ng'ombe ndani ya zizi. Walikunja ngumi wakitegeana.

    "Niliwapa onyo, naona hamjataka kulisikia!" Alisema Jona akimkazia macho Kinoo.

    "Wewe si wa kutupa sisi onyo. Bado huna hadhi hiyo," Kinoo akajibu kwa dharau kabla hajaguna.

    Jona akatabasamu asitie neno. Alipanga matendo yake yaongee sasa na si sauti ya mdomoni.

    Kimwili alikuwa mdogo ukimlinganisha na Kinoo, na alijua hilo lina faida na hasaraze. Endapo akiingia mikononi mwa Kinoo basi itamuwia vigumu kuchoropoka.

    Faidaye, Kinoo atakuwa mzito kufanya mashanbulizi. Miili mikubwa huchukua hatua kubwa kushurutisha viungo.

    Basi akajipanga vema kutumia hiyo faida.

    Akachokoza pambano kwa kurusha ngumi mbili za haraka, Kinoo akazikwepa kisha akatuma ngumi yake nzito. Jona akayeya! Ikapita.

    Akatuma nyingine na nyingine, Jona akazikwepa kama mchezo wa rede.

    Kwa nusu dakika, akausoma mchezo, akapata alichokuwa anakitaka.

    Kinoo hakuwa mzuri kwenye kujilinda, alikuwa mzito kukwepa, na alikuwa akiziacha mbavu zake wazi mara kwa mara.

    Bila shaka alikuwa anategemea zaidi kushambulia kuliko kujilinda.

    Jona akaanza kucheza na mbavu za mwanaume huyo, akilenga kumtepetesha na kumminya uwezo wa kuhema.

    Kinoo akarusha ngumi zake kwa mfululizo, Jona akawa anakwepa kisha anakita mbavu za Kinoo kwa ngumi za upesi.

    Kila alipopata mwanya, basi akafyatua ngumi tatu ama nne!

    Ikafikia mahala Kinoo akachoka kwani alikuwa anatumia nguvu nyingi kurusha ngumi zilizokuwa zinaenda patupu. Ukijumlisha na ngumi alizokuwa antekenywa mbavuni, akashindwa kufua dafu.

    Alikuwa hoi bin taaban.

    Alikuwa anatamani kuhema kwanguvu, lakini mbavu haizikuruhusu. Ni kama vile alipewa pumu.

    Ni wazi alikuwa ameshindwa, ila hakutaka kuingia kwenye mikono ya adui, hivyo basi akatoroka kwa kukimbia.

    Aliruka ukuta akazama ndani ya gari lake na kuhepa kwa kasi!

    Jona alihofia kufyatua risasi kutoshtua majirani. Hakutaka kuwapa hofu wala makisio na mahisio yoyote juu yake na mambo yake.

    Basi akamwacha Kinoo aende. Huko akafikishe habari aliyokumbana nayo.

    Yeye akarudi zake ndani na kumtazama Bigo. Akampuuzia na kuendelea na mambo yake. Akaoga na kisha akajipeleka chumbani alipojilaza akiendelea kunywa.

    Bigo aliachwa palepale kwenye kiti.



    ***



    Kadiri usiku ulivyokuwa unasonga ndivyo na tafrija ilivyokuwa inanoga.

    Sasa ilikuwa ni saa tano inayoelekea saa sita usiku na muziki laini ulikuwa unaburuza eneo wageni wakiserebuka.

    Ndani ya eneo hili lililokuwa limesheheni taa kali zilizogeuza usiku kuwa mchana, kulikuwa kuna walinzi kedekede wakiwalinda wanaume na wanawake waliokuwa humo tafrijani.

    Watu hawa walikuwa ni 'vibopa', watu wazito wenye nyadhfa zao serikalini ama mahala pengine nyeti kiuchumi.

    Karibia wanaume wote walikuwa wamevalia suti, zikipishana tu rangi. Wanawake 'wakila' magauni ya kupendeza na michuchumio ya haja.

    Nyuso za wanawake hawa zilikuwa zimerembwa kwa 'make-up' zilizofiti usoni. Waling'aa kama malaika, ila hawagusa kwa mwanamke Miranda.

    Alikuwa amependeza haswa. Pia na kujiamini kwake pamoja na kujua kwenda na muda, kulimfanya avutie zaidi.

    Kila muziki ulipowekwa alijua kwenda na mapigo. Alifanya watu wamtazame na pia kumwongelea wasijue mwanamke huyu alikuwapo kazini, na lengo lake lilikuwa kumtia kimyani mheshimiwa fulani.

    Muziki ulikata, wakarejea kwenye viti vyao. Miranda alikuwa ameketi na BC meza moja. Meza iliyokuwa imechafuliwa kwa vinywaji.

    Meza yao ilikuwa inatazamana, kwa umbali kidogo, na meza aliyokuwa ameketi mheshimiwa Boka, waziri wa Afya. Mwanaume mnene mweusi mwenye kitambi kama kiroba cha mihogo.

    Alikuwa amevalia suti na tai ya bluu. Mezani alikuwa pamoja na mwanamke fulani mnene, pasi shaka mkewe, pia na kijana mmoja wa kiume mwenye kadirio la miaka ishirini na saba - nane - tisa.

    "You did great!" (Umefanya vizuri!) BC alisema akitazama meza ya mheshimiwa Boka. "He was really impressed, now we've to figure the way out to reach him." (Aliguswa sana, sasa tunatakiwa tutafute njia ya kumpata.)

    "The problem is his wife," (shida ni mkewe,) alisema Miranda akikunja shingo kutazama penye lengo. "She's very close to him as if she knows our intention. But I will get the way out!" (Amemganda sana kana kwamba anajua lengo letu. Lakini nitapata namna!)

    Miranda aliposema tu hivyo, akanyanyuka akijifanya anatengenezea nguo yake vizuri. Mheshimiwa akamtazama, naye akamtazama kukutanisha macho.

    Akatabasamu na kutazama kiaibu. Mheshimiwa naye akatabasamu kujibu.

    Miranda akaketi. Sasa akajua dhahiri mheshimiwa Boka atakuwa anatazama tazama mezani kwake baada ya hilo tukio.

    Basi hakujiweka mbali. Akawa anampa mheshimiwa macho na kajitabasamu.

    "The bird's fallen into the trap!" (Ndege ameangukia mtegoni!) Akasema Miranda kwa tabasamu.

    "Now take it!" (Sasa mchukue!) BC akashadadia.

    Punde Miranda akanyanyuka, akamtazama mheshimiwa, kisha akayaelekezea macho yake upande wa maliwatoni.

    Alafu akaelekea huko akitembea kwa madaha ya walimbwende jukwaani. Mheshimiwa akamsindikiza kwa macho ya ukware.

    Naye, isichukue muda, akanyanyuka aende huko huko maliwatoni. Basi wakakutana na Miranda kwenye korido.

    Mwanamke huyo alikuwa anahangaika na zipu ya gauni huko mgongoni, akijinasibu anahangaika kuifunga.

    "Naweza nikakusaidia?" Mheshimiwa Boka akapaza sauti akitabasamu.

    'Naona umejileta mwenyewe boya wewe!' Miranda akasema kifuani. Aligeuza uso wake kutazama, akakutana uso kwa uso na waziri. Akaigiza aibu.

    "Hapana, ahsante mheshimiwa," akajibu akitabasamu.

    "Aaaah bwana mrembo kwanini upate shida hivyo na mie nipo?"

    Miranda hakusema kitu. Alitabasamu tu akaendelea kuhangaika na zipu yake. Basi mheshimiwa akaamua kujisogeza, alichukulia ukimya kama 'ndio', akadaka zipu ya Miranda na kuipandisha juu pasi na tabu.

    "Ahsante sana, mheshimiwa, na samahani kwa usumbufu!"

    "Usijali, mrembo. Unaitwa nani wewe?"

    "Flaviana," Miranda akajibu akitazama chini.

    "Oooh jina zuri kweli!"

    "Ahsante."

    Mheshimiwa akatazama mazingira, akajiona wapo wenyewe. Ila alijua fika hawatadumu kwa muda mrefu hapo. Aidha mkewe aje, ama watu wengine waliobanwa na haja, basi akaamua afanye mambo upesi.

    "Sasa mrembo nataka tupate nafasi ya kuongea vizuri na wewe. Vipi sasa nitakupataje? - una simu?"

    "Ndio ninayo."

    "Sawa sawa!" Mheshimiwa akajipekua mfukoni, akatoa kadi ya biashara na kumkabidhi Miranda.

    "Utan'chek basi, sawa?"

    Miranda akatikisa kichwa. "Sawa, mheshimiwa, n'tajitahidi."

    Mheshimiwa akatabasamu na kujilamba lips, akatoka maeneo ya maliwato na kurudi kwenye meza yake.

    Baadae kidogo napo Miranda akarudi zake kukutana na BC. Akamwonyeshea kadi aliyopewa na mheshimiwa.

    "That's a very big step!" (Hiyo ni hatua kubwa sana!) BC akasema akimpongeza Miranda kwa kumpa mkono. "We have already put him in our store." (Tayari tumeshamtia kwenye ghala.)

    Sasa wakanywa kwa furaha wakiendelea kupanga na kusuka mipango yao.

    Walikuwa na matumaini makubwa ya kumtia mikononi mheshimiwa Boka, na lengo lao kuu ni kumtumia kiongozi huyo wa kitengo cha Afya kusafirisha mizigo yao kwa kutumia kibali chake.

    Huyu kwake alikuwa na faida kubwa kuliko mheshimiwa Eliakimu kwani yeye anahusika moja kwa moja na mambo ya madawa.

    Lakini pia gharama yake itakuwa ndogo ama hamna kabisa kwasababu ya kumtumia Miranda kama chambo.

    Wakiwa wanelekea ukingoni wa tafrija na sasa wakiwa wanajiandaa kuondoka zao,kwa amani kabisa maana hawajaupoteza usiku, mara kwa mbele yao wanamuona mke wa Mheshimiwa Boka akija.

    Kabla hawajafanya kitu, mwanamke huyo alikuwa mbele yao akishikilia kiuno.



    “Habari binti?” alimsalimu Miranda, kisha akatabasamu.



    “Safi, sh’kamoo.”



    “Marhaba, umenifurahisha sana. Umeufanya usiku wangu kuwa wa kumbukumbu.”

    Miranda akatabasamu.



    “Nashukuru sana mama.”



    “Usijali, sasa kuna jambo moja nilikuwa nataka tutete mimi na wewe, ningepata faragha?” Alisema mke wa mheshimiwa akimtazama BC. Miranda naye akamtazama BC kabla hajajibu akipandisha mabega.



    “Sawa, hamna shida.” Kisha wakasogea kando kidogo.



    “Sina malengo ya kukuvunjia heshima, ila nimependezwa nawe na nikaona nastahili kukushirikisha hili kama utakuwa umevutiwa. Unapendelea mambo ya modeling na ulimbwende?”



    “Aaaahmm …kiasi.”



    “Nina kampuni ya ulimbwende na modeling ambayo inahusika moja kwa moja na mambo ya vipodozi na marashi. Ningependa kufanya kazi na wewe.”



    Kidogo Miranda akabanwa na kigugumizi.



    “Sitaki unipe jibu lolote kwa sasa, ni jambo nililokushtukiza. Chukua muda wako na ufikirie, utanipatia jibu.”



    Mke wa mheshimiwa akafungua pochi yake, akatoa kadi na kumkabidhi Miranda.



    “Unajua sikuwa na wazo lolote lile mpaka pale mume wangu aliponishtua na kunishauri. Ni kweli nilivutiwa nawe sema akili yangu ilikuwa kiparty-party zaidi.” Mke wa mheshimiwa alinena akitabasamu.



    “Ahsante sana, mama. N’taona namna itakavyokuwa,” akasema Miranda kisha wakapeana mikono na kuagana. Miranda akamrudia BC wakaondoka zao kuelekea kwenye gari.



    Miranda akamueleza BC juu ya yale mke wa mheshimiwa aliyomwambia.



    “It might be an opportunity.” (Yaweza kuwa fursa) BC alisema akitazama mbele, kisha akauliza: “Do you have any helpful idea from that?” (Una wazo lolote lenye tija toka kwenye hilo?”

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Miranda akaminya lips. “Perhaps it may spark later, but for now I take it as a chance for me to be officially closer to Mr. Boka.” (Pengine laweza kutokea baadae, lakini kwa sasa naichukulia kama fursa ya mimi kuwa rasmi karibu na bwana Boka.)



    “Yes, but you never know as you will be closer to the wife as well. This game becomes very thrilling, we have to win something out of it!” (Ndio, lakini huwezi jua maana utakuwa karibu na mke vilevile. Huu mchezo unakuwa mzuri zaidi, na tunatakiwa kushinda jambo toka kwenye hilo!”



    Miranda hakusema kitu, alikuwa kimya akitafakari.



    Gari lilinguruma pasipo watu kuongea mpaka wanafika getini mwa makazi ya Miranda ambapo wanaagana, na Miranda anaingia ndani baada ya kufunguliwa mlango na mlinzi.



    “Kuna mgeni yoyote amekuja hapa?”



    “Hapana, mam, hamna!”



    “Kabisa?”



    “Ndio, yupo tu Kinoo.”



    “Sasa huyo si mgeni?”



    “Samahani, mam, nilidhani labda unaulizia mgeni mgeni yani…”



    “Amekuja saa ngapi?”



    “Mida kama ya saa tatu hivi kama nipo sahihi.”



    “Hajaja na gari?” Miranda aliuliza akiangaza angaza.



    “Hapana, alikuja na bodaboda.”



    “Alikuwa amebebelea kitu chochote mkononi?”



    “Hapana, sijaona zaidi ya simu.”



    Miranda akasonya, kisha akanyoosha hatua zake ndefu kuelekea ndani. Alimkuta Kinoo akiwa amejilaza juu ya kiti akijikunyata kana kwamba anahisi baridi kali. Usoni mwake alikuwa na majeraha, na hakuwa nadhifu.



    Akamwamsha.



    “Vipi, mbona hivi? – umechukua picha?” Akauliza maswali kwa mkupuo. Kinoo akayajibu kwa kutikisa kichwa chake kukataa. Hakutia neno.



    “Hujafanikiwa?” Miranda akatahamaki. Alikunja sura yake na kushika kiuno. Akashusha pumzi ndefu kabla hajakaa.



    Yalikuwa ni majira ya saa nane usiku sasa. Kulikuwa kimya, kwa mbali kulikuwa kunasikika vijisauti vya vijibwa vikibweka.



    “Sijafanikiwa kupata picha,” alisema Kinoo akitazama chini. Alimweleza Miranda namna mambo yalivyotukia ndani ya eneo la tukio. Miranda akashangazwa.



    “Nilikuambia Kinoo, na hukutaka kunisikia!”



    “Nini sijakusikia?”



    “Nilikwambia yule si msanii tu wa kawaida, ni mtu mwenye mafunzo na ujuzi. Ila wewe ukapuuzia, kwa namna ulivyomshambulia ni kana kwamba ulienda kumkamata konda wa daladala!”



    Kinoo hakusema kitu, alikuwa anatazama tu chini.



    “Huyu mtu ni nani?” Miranda aliuliza akisimama. Aliweka mikono yake nyuma akitambaa na tafakari. “Huyu mtu ni nani haswa? Ni mchoraji tu? Kwanini Bite alimchagua kufanya naye kazi? Kutakuwa kuna sababu yoyote ama ni bahati tu?” Miranda aliteswa na maswali.



    Kinoo alimtazama akamwambia:



    “Kama ulivyosema hapo awali, mchoraji atakuwa anafuatiliwa na wale watu waliokuja hapa kuteka kamera. Na pasipo na shaka, wao ndiyo watakuwa wanahusika na mipango ya kumuua kwa kutumia gari kama mchoraji alivyokuja kushtaki hapa.”



    “Wanataka kumuua,” Miranda alisema akitikisa kichwa. “Wanataka kummaliza, ina maana wanajua mchoraji huyo ana picha hatarishi kwao.”



    “Ndio.”



    “Sasa tutapataje picha Kinoo? Picha hiyo muhimu sana!”



    “Nina wazo – kwanini tusikae meza moja tukaongea na mchoraji yule?”



    “Oooh umeona sasa kile nilichokuwa nasema – si kila mara nguvu yatakiwa. Lakini mashaka yangu ni kwa huyo mchoraji, sijui kama atakubali.”



    “Nadhani ameshajua sisi hatuhusiki na jaribio la kumuua, anaweza kukubali.”



    “Sawa, ila akikubali atataka kujua kuhusu hiyo picha. Atataka kufahamu ina nini na kwanini inatafutwa. Huoni kama hilo ni tishio?”



    “Kwani akijua kuna nini?”



    “Hapo ndipo mimi naanza kushindwana na wewe. Wewe unajua kilichomo kwenye ile picha?”



    “Hapana.”



    “Unajua imechorwa nini?”



    “Labda…”



    “Labda nini? Hatuna uhakika, na pengine tunaweza tukaipata na bado tukashindwa kuing’amua. Endapo kama ina siri kubwa, na ndivyo inavyoonekana kutokana na utafutwaji wake, tutafanyaje? Tutamuua?”



    Kinoo kimya.



    “Ebu niache nilale. Siku ya leo ilikuwa ndefu sana kwangu,” Miranda alisema akielekea zake ndani ya chumba.



    Hakutoka.







    ***







    “Leo unaonekana upo bize kweli ndugu yangu,” Jumanne alimwambia Jona akimshika bega.



    Yalikuwa ni majira ya saa mbili asubuhi ndani ya ofisi. Siku ilikuwa imejazwa na shughuli kama kawaida. Magari lukuki yalikuwa yanakatiza huko barabarani kama ilivyo kwenye barabara nyingi ndani ya jiji la Dar es salaam.



    “Ni kweli, nimetingwa kidogo,” Jona akamjibu Jumanne pasipo kumtazama. Siku hiyo alikuwa amekuja na tarakilishi yake mpakato na ndiyo alikuwa anahangaika nayo tokea alipokuja.



    Pembeni ya tarakilishi hiyo kulikuwa kuna kakibahasha kadogo cheupe, ndani yake kulikuwa kuna picha aina ya pasipoti. Picha moja ilikuwa imetokezea kwa nje.



    Jumanne alikuwa anataka kutoka akapate kifungua kinywa, ila akaangaza kidogo alichokuwa anakifanya mwenzake, kile kilichomchukulia muda namna ile.



    Akaona Jona yupo mtandaoni, akisoma soma baadhi ya Makala na kupitia baadhi ya picha. Jumanne akapuuzia, ila kabla hajaenda, akaona picha ile iliyokuwa imejitokeza toka kwenye kibahasha.



    Aliitazama picha hiyo kwa umakini, haikuwa ngeni. Aliisogelea akaikodolea vema kabla hajamwomba Jona ruhusa ya kuichukua na kuisogeza machoni.



    “Unamjua huyo mtu?” Jona akamuuliza Jumanne. Kwa mara ya kwanza aliacha mashine yake akamtazama mwenzake.



    “Nahisi kama namjua. Umeitoa wapi?”



    “Kuna mtu tu amenipatia. Vipi? – ulimuonea wapi?”



    Jumanne alivuta kiti akaketi. Akaendelea kutazama picha hiyo akivuta kumbukumbu.



    “Oooh! Sasa nimekumbuka.”



    “Ni nani?”



    “Huyu ni marehemu Fakiri – aliyewahi kuwa mfanyabiashara mkubwa wa samaki. Alikuwa anasafirisha samaki wa maji chumvi mikoa yote ya Tanzania. Mpaka huko Kongo, Rwanda na Burundi.”



    “Ni marehemu?”



    “Ndio. Aliuawa mwaka jana.”



    “Aliuawa na nani?”



    “Aaaah Jona! Unadhani mie n’tajulia wapi sasa? Nawe waniuliza maswali utadhani kachero wa polisi.”



    Jona akatabasamu pasipo kutia neno.



    “Mie naenda kunywa chai, mzee. Baadae,” Jumanne aliaga akaenda. Joh akaichukua ile picha aliyokuwa anaitazama Jumanne, akaitazama na yeye.



    “Fakiri …” Jona alijikuta anaongea mwenyewe. Alitazama nyuma ya picha, akaona maandishi yale ya kichina ambayo yapo kwenye picha zote.



    Akaweka picha pembeni na kurejea mtandaoni kwenye injini ya kusaka majibu. Akaandika: ‘Mauaji ya Fakiri’ alafu akabonyeza kitufe cha ‘ok’. Punde majibu yakaja kibao, akaanza kuyapitia moja baada ya moja.



    Fakiri aliuawa kwa kunyongwa siku ya tarehe 12, desemba 2016 maeneo ya nyumbani kwake Masaki. Ameacha mjane na mtoto mmoja, ambaye naye alikuja kuuawa juma moja tu baada ya baba yake, yeye akiuawa kwa risasi.



    Mpaka sasa hakuna yeyote anayeshikiliwa na polisi kwa mauaji hayo.



    Kama juma moja hapo nyuma kabla ya Fakiri kuuawa, alikuwa akikabiliana na kesi ya ukwepaji kodi. Kesi ambayo ilikuwa inaelekea kumshinda na hivyo basi kutakiwa kulipa limbikizo kubwa la kodi pamoja na faini kubwa. Kwa jumla shilingi za kitanzania milioni mia tano! – nusu bilioni.



    Pengine ungweza kudhani Fakiri alijiua kwasababu ya kukwepa fedheha hiyo ya biashara yake kufia mikononi, ila hakujiua! Aliuawa! Ni wazi serikali isingeweza kumuua mtu wanayemdai, tena pesa kubwa hivyo.



    Sasa nani alimuua? Na alifanya hivyo kwa malengo gani? Na kwanini mtoto wake naye akauawa? Maswali hayo hayakuwahi kupata majibu toka upande wowote ule.



    Ila juu yake hayo, Jona anapata tena swali lingine, mbona picha ya Fakiri ilikuwa ndani ya kibahasha cha Bigo? Ina maana yeye ndiye anahusika na mauaji hayo? Kama ndio, mbona ya mtoto wa Fakiri haipo? Yeye aliuawa na nani?



    Akajikuta anashusha pumzi ndefu baada ya kuona ana mlima mkubwa wa kuupanda. Lengo lake lilikuwa ni kumjua tu Bigo ni nani na nani aliyemtuma ila anajikuta anagundua mambo mengine ambayo hakutaraji.



    Ayaache? Hapana! Haya mambo yanaweza kumsaidia akaunganisha doti kumjua Bigo hasa ni nani na anamfanyia kazi nani.



    Lakini juu ya yote haya, kwanini hawa watu wanataka kumpoteza? Kosa lake ni nini?



    Kama angelikuwa bado yu ndani ya jeshi la polisi, basi angesema aliingia kwenye anga zao, ila la hasha! Sasa tabu nini? Alishawahi kuwagusa watu hawa pindi akiwa jeshini? Akajiuliza. Mbona hawakumtafuta muda wote huo?



    Masikini hakujua chanzo ni picha. picha tu ndiyo ambayo inataka kumtoa roho. Picha tu ndiyo ambayo inamwingiza kwenye anga la wababe wanaotaka kunyofoa uhai wake kama vile Bite.



    Jona anarudishwa ndani ya ulingo wa mapambano pasipo kutarajia. Anarudishwa kazini japokuwa alishakataa hii kazi aendelee na maisha mengine.



    Kabla ya kuendelea kuperuzi na kuhangaika juu ya Fakiri, kwanza akapata wazo la kuyatambua yale maneno yaliyokuwepo nyuma ya pasipoti zote za Bigo.



    Kwa kutumia alama za kichapio cha tarakilishi zake, anakopi maneno yale kwenye injini ya kusakia majibu mtandaoni kisha anasaka.



    Punde yanakuja majibu mengi, anachagua jibu moja na kuliangaza. Anaona maneno matatu: ‘Pumzi ya mwisho’. Kumbe ndiyo maana ya yale maneno.



    Moja kwa moja akajihakikishia kumbe wale watu kwenye pasipoti walikuwa kwenye ahadi ya mauaji. Maana yake walikuwa kwenye pumzi zao za mwisho.



    Kwanini wauawe? Na ni nani aliyekuwa anataka kuwaua?



    Pasipoti zilikuwa mpya mpya. Hilo lilimaanisha orodha hiyo ya mauaji haikuwa ya zamani. Yani kama kwa kukadiria, ina mwaka tu, kama ikizidi ni miezi tu kadhaa.



    Kwahiyo wote waliokuwa kwenye pasipoti wameuawa? Au kuna wengine bado wapo hai? Kwanini yeye hayupo kwenye pasipoti ila analengwa kuuawa?



    Akili yake ikamwambia yeye alitokea tu kwa dharura, kuna watu waliokuwa kwenye orodha tangu kitambo. Ni nini basi hicho kilichomwingiza kwenye orodha?



    Maswali yalizidi kichwa, akaona anahitaji kupumzika. Aliachana na tarakilishi yake kabla hajaidaka simu na kwenda zake nje aliposimama na kuangaza barabarani kana kwamba anahesabu idadi ya magari.



    Alitaka kutoka akajipatie kikombe cha chai ila ofisi amwachie nani? Jumanne bado hakuwa amerudi.



    Hali hiyo ikamlazimu ang’ae ng’ae macho kabla ya muda kidogo simu yake haijatetemeka kumwashiria ujumbe umeingia. Akaichomoa na kuitazama. Ni ujumbe wa Facebook toka kwa Miriam – mke wa mheshimiwa Eliakimu.



    Jona akatabasamu.



    ‘I think I need your phone number if you don’t mind’ (Nadhani nahitaji namba yako ya simu kama hutojali’



    ‘It’s just ok, I wanted to ask for it earlier but hesitated.’ (ni sawa, nilitaka kukuomba hapo mapema lakini nikasita.’



    Chati yake na Mariam zilionekana hivyo. Yeye alikuwa wa kwanza kutuma ujumbe kuhusu kuomba namba ya simu kabla ya hajajibiwa na Miriam kwamba naye pia alikuwa anataka kuomba.



    ‘Did you fear to ask?’ (Uliogopa kuomba?)



    ‘Somehow, you know. You were impressed so I decided to wait.’ (Kiasi, si unajua. Ulikuwa umevutiwa kwahiyo nikaamua kungoja.)



    Jona akatuma vimdoli vya kutabasamu, na ndiyo hivyo punde namba ikatumwa na Miriam.



    ‘At what time am I supposed to find you?’ (Kwa muda gani natakiwa kukutafuta?) Jona akautuma ujumbe kuuliza. Uzuri Mariam alikuwa mtandaoni hivyo akajibu upesi:



    ‘At any time.’ (Muda wowote.)



    ‘Really?’ (Kweli?)



    ‘Yah! Why asking?’ (Ndio! Kwanini unauliza?) Mariam aliambatanisha ujumbe wake na vimdoli vya kushangaa.



    ‘I didn’t expect that ‘anytime’, aren’t you in relationship? Sorry for asking though.’ (Sikutegemea hiyo ‘muda wowote’, haupo kwenye mahusiano? Samahani kwa kuuliza lakini.)



    ‘Don’t mind, I am not in relationship that’s why I am free’ (Usijali, sipo kwenye mahusiano ndiyo maana nipo huru.)



    ‘Better for you! Expect my call n’ messages soon!’ (Ni njema kwako! Tegemea simu na jumbe zangu karibuni!)



    ‘Wow! Can’t wait.’ (Wow! Nangoja kwa hamu.)



    Jona akatoka huko mtandaoni baada ya kuinakili namba ya Bite kichwani, akaitunza kwenye simu yake kwa jina la ‘target no.1’. Kabla hajaendelea zaidi, Jumanne akarejea, basi yeye akaenda kujipatia chai angalau atie joto tumboni.



    Akiwa anangoja kikombe cha chai, akaendelea na kazoezi kake.



    Akahamishia namba ya Miriam kwenye msako wa lokesheni kwa kutumia GPS. Simu ikaanza kutafuta taratibu. Mara ikaeleza wapi namba ya Miriam inapopatikana.



    Jona akajikuta anatabasamu.



    “Hadithi imeishia hapa,” akanena mwenyewe.



    “Hadithi gani?” mara sauti ikamuuliza na kumfanya atoe macho yake kwenye simu. Alah! Alikuwa mama K akiweka kikombe cha chai mezani.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Masikio yako yapo kazini muda wote mama K!”



    “Kama ilivyo mikono yangu,” mama K akajibu kwa tabasamu, kisha akasema: “Jumanne alisema utakuja.”



    “Wapi?”



    “Kuna mahali pengine zaidi ya hapa?” Alijigamba mama K ndani ya gauni lake la kale lenye mistari hafifu rangi ya kijani. Nywele zake alikuwa amezifumba na kiremba kikubwa cha pande la khanga, miguu yake ndani ya raba za pinki.



    “Amesema ukija utamlipia chai aliyokunywa.”



    “Mimi?”



    “Sasa hapa naongea na nani? Au sio Jona wewe?”



    “Jumanne pumbavu kabisa!” alisema Jona akitikisa kichwa. “Anajifanya mjanja unh?… usijali, n’talipia!”



    Mama K akatabasamu kisha akaenda zake.



    Akiwa mgahawani, Jona hupenda kukaa mahali panapoweza kumfanya akaona ofisi yake. Hufanya hivi ili asije akakosa ama kupitwa na taarifa yoyote ile toka upande ule wa pili.



    Akiwa anakunywa zake chai taratibu, kichwani akiyapangilia mafaili, kwa mbali alikuwa anatazama ofisi na kushuhudia wageni watatu wazungu wakizama ndani.



    Jumanne aliwapokea kwa bashasha na punde akaanza kuwaonyesha bidhaa kwa mikono yake iliyokuwa inapanda na kushuka, ikienda kushoto na kulia.



    Mpaka Jona anamaliza kunywa chai, wageni walikuwa tayari wameondoka.

    Alishika zake njia kurudi ofisini.



    Kabla hajafika, ikiwa imebakia takribani kama hatua tatu tu, Jona anamuona mwanamke fulani upande wake wa kushoto hatua kama kumi na tatu kwa umbali.



    Mwanamke huyu alikuwa amevalia sketi fupi, topu, koti fupi dogo la kung’aa, viatu virefu vinayokomea magotini, miwani ya jua na wigi refu. Vyote hivi vilikuwa vyeusi kwa rangi!



    Mkono wake wa kuume ulikuwa umebebelea simu kubwa. Alikuwa amesimama akichezea hii simu. Ila Jona aliporusha macho yake upande wake, haraka akageuzia sura yake pembeni.



    “Nishawahi kumwona huyu mwanamke wapi?” Jona alijiuliza akiingia ndani ya ofisi. Kimo, rangi na shepu ya mwanamke yule kwake havikuwa vigeni. Japokuwa sura hakuwa anaifahamu, ila ‘kapicha’ kalikuwa kyenyeji.



    Aliipokutana na Jumanne na kuanza kuongea kuhusu ya mgahawani, akili yake ikampuuzia na kumsahau mwanamke huyo.





    ***





    Kwenye majira ya saa mbili usiku: Mbweni.





    Mazingira yalikuwa na rasha rasha za vijikelele vya hapa na pale kama mara nyingi inavyokuwa kwenye nyumba za kupanga ambazo zimesongamana pamoja.



    Katika eneo hili, kaya nne zilikuwa ndani ya uzio mmoja mkubwa, kila nyumba ikiwa imejitenga mbali kidogo na mwenzake. Nyumba hizi zilikuwa zinafanana kuanzia rangi mpaka mpangilio wake.



    Kama mtu ni mgeni wa eneo basi unaweza kupotea ukachanganya milango.



    ‘Nisubirie hapo hapo nakuja,’ Kinoo aliyekuwa amesimama getini, kwa ndani, aliupokea ujumbe huo simuni. Akangoja.



    Alikuwa amevalia ‘kibody’ cheusi, suruali ya jeans na raba nyeupe.



    Punde anamwona Mudy, mwanaume yule aliyekuwa anafanya kazi kwenye kampuni ya Bite, akija. Alikuwa amevalia jezi ya mchezo wa mpira ya taifa la Hispania. Mkononi alikuwa ana simu.



    Alimpokea Kinoo wakaongozana naye kuelekea nyumba ya upande wa kushoto mwa geti, kwa nje kulipaki Rav4 nyeupe. Wakazama ndani na kujiweka sebuleni. Baada ya maongezi mafupi, Mudy akaenda chumbani na kurejea na faili moja kubwa rangi ya samawati aliloliweka mezani.



    “Kuna nyaraka fulani ya malipo, Bite aliniachia wiki moja kabla ya mauaji yake. Nakumbuka alinisisitizia sana niahakikishe natuma pesa kwenda kampuni fulani ya kusambaza umeme wa jua.”



    Mudy akaonyesha nyaraka hiyo kwa Kinoo.



    “Ilikuwa kiasi kikubwa sana cha pesa. Ila nilikuwa nimetingwa na kazi nyingi na hata kupelekea kupita siku tatu nikiwa sijatuma pesa hiyo. siku ya nne, Bite alikuja akiwa na mashaka na haraka akaniuliza kama nimetuma ile pesa, nikamwambia hapana lakini nikihofia sana huenda atanikaripia kwani alisisitiza.



    Ajabu, akafurahi. Akanambia: ‘Ahsante sana Mudy, usitume tena hiyo pesa. Hao watu ni mafedhuli wakubwa, wezi na wauaji. Acha mara moja!’ kisha akaenda zake.



    Huoni kampuni hii ndiyo watuhumiwa namba moja na sababu ikawa ile pesa?” Mudy alimalizia taarifa yake na swali. Kinoo akaunga mkono hoja.



    “Ni kweli kabisa!” kisha akauliza: “Na vipi Brokoli? – alichukuliaje hii taarifa?”



    Mudy akapandisha mabega juu.



    “Sijui! Ila nakumbuka walikaa vikao viwili kama si vitatu mfululizo. Hatukuambiwa wanaongelea nini. Wala hatukupashwa habari kama kuna mabadiliko ama mazingatio yoyote kutokana na vikao hivyo!”





    Kinoo akaguna kisha akauliza:



    “Unajua wapi Brokoli anaishi?”



    “Yah! Najua,” Mudy akajibu akitikisa kichwa.



    “Na ulishawahi kuiftuatilia hiyo kampuni ya umeme wa jua?”



    “Hapana. Sikufanya hilo kwa kutegemea polisi watalivalia njuga.”



    “Sawa, na vipi kama hili jambo likabuma tena huko polisi, upo radhi kwenda umbali gani kutafuta haki ya Bite?”



    Kidogo Mudy akasita.



    “Una maanisha nini?”



    “Unajua Mudy, si kila muda mambo yanaenda kama vile tunavyotarajia ama tunavyotaka. Nadhani uliona namna polisi walivyokuangusha ulivyowapelekea hili jambo. Sasa mimi nataka kujua unaweza kwenda kilomita ngapi kutafuta haki ya Bite?”



    “Kadiri ya uwezo wangu.”



    “Ahsante sana, hicho ndicho nilikuwa nataka. Njia hii inaweza ikawa ngumu na ndefu, inabidi tujiandae. Aidha kupita njia kuu ama nyinginezo ilimradi haki ipatikane.”



    Kinoo akasafisha kwanza koo, akaendelea:



    “Kikubwa ninachohitaji toka kwao ni taarifa tu, hayo mengine mimi nitayasimamia. Nitahitaji taarifa mbalimbali toka ofisini mwenu kama hutojali, yote kwa ajili ya Bite.”



    “Nitajitahidi kadiri ninavyoweza.”



    Wakapeana mikono. Kinoo akaaga.



    “Ina maana mgeni unaondoka pasipo kupata chochote kitu?”



    “Nashukuru sana, usijali. Leo si mwisho wa dunia. Anyway, unaishi mwenyewe?”



    “Yah! Nipo mwenyewe.”



    “Nyumba yote hii?”



    Mudy akatabasamu. “Ndio, nipo mwenyewe.”



    “Aisee!” Kinoo akatahamaki akiangaza huku na huko. Akapandisha mabega yake na kupinda mdomo.



    “Haya mzee. Ningependa unipatie hizi nyaraka zako nikajaribu kufuatilia baadhi ya mambo. Pengine naweza nikaibuka na jambo.”



    Mudy akamkabidhi.



    “Kuwa makini, bado zinahitajika na ni muhimu ofisini.”



    Kinoo akaitikia kabla hajaenda zake. Cha kwanza alichokifanya ni kumtafuta na kukutana na Miranda. Alikuwa yupo nyumbani kwake akijipatia kinywaji laini na kutazama televisheni. Alikuwa amevalia bukta ya timberland na blauzi nyeusi.



    Akamweleza yale yote aliyoyapata huko kwa Mudy.



    “Umefanya kazi nzuri!” Miranda akampongeza akipitisha pitisha macho yake kwenye nyaraka alizokuja nazo Kinoo.



    “Lakini … Kinoo, kama vile naijua hii kampuni.”



    “Serious?”



    “Yah! Serious.”



    “Ipo wapi?”



    “Kama sijakosea, nilishawahi kuiona ikitangazwa kwenye TV. Tena si zamani, jana tu! … ngoja!” Miranda akanyaka rimoti na kubadili alichokuwa anakitazama toka kwenye movie mpaka chaneli ya kawaida.



    “Bila shaka niliona hilo tangazo hapa.”



    Alipoweka hiyo chaneli, wakaendelea na maongezi mengine. Wakagusia swala la picha ya Bite iliyopo kwa Jona.



    “Nimeona ni vema nikaonana naye binafsi,” alisema Bite akikuna kichwa. “Nadhani nikimwelezea vizuri anaweza akanielewa. Hata kama asiponipa hiyo picha basi anipe wasaa mdogo wa kuitazama.”



    “Unadhani atakukubalia?” Kinoo akauliza.



    “Hayo yote ni matokeo: kunikubalia ama kunikatalia. Ila angalau nimejaribu. Lakini najua sitashindwa.”



    Kinoo akaguna.



    “Labda … sijui.”



    “Kuna utofauti kati yangu na wewe,” Miranda akasema akimtazama Kinoo. “Tofauti moja kubwa mimi ni mwanamke na wewe ni mwanaume.”



    Mara simu ya Miranda ikanguruma na kukatisha maongezi. Miranda akaitazama kujua ni nani kabla hajaiweka sikioni. Alikuwa ni waziri wa michezo; Mheshimiwa Eliakimu Mtaja.



    “Tunaweza tukaonana, binti?” sauti ya Eliakimu iliuliza.



    “Muda gani mheshimiwa?”



    “Kesho majira ya jioni hapa nyumbani kwangu.”



    “Sawa.”



    Simu ikakata. Lakini ilimkumbusha jambo, kuwasiliana na bwana Boka, waziri wa Afya. Alienda chumbani kwake akarejea na kadi ya biashara aliyopewa na mwanaume huyo, akapiga namba iliyokuwa imeanishwa.



    Bahati haikuwa kwake, simu haikupokelewa. Alipiga mara tatu kabla hajaamua kusitisha zoezi hilo.





    ***





    “Kesho atakuja,” alisema bwana Eliakimu akimwambia Nade. Wote walikuwa sebuleni peke yao. Sauti ya televisheni ilikuwa inanguruma kwa mbali ikikosa shabiki wa kuitazama.



    Eliakimu alikuwa amevalia suti ya traki ya michezo rangi ya bluu, Nade akiwa amejivalia suruali nyeusi ya kitambaa iliyoendana na koti lake fupi jeusi lenye kola rangi ya pinki.



    “Nadhani mipango yetu imeenda kama tulivyotarajia,” alisema bwana Eliakimu. Nade akatikisa kichwa.



    “Ndiyo, mkuu. Lakini kuna kajitatizo kadogo kametokea.”



    “Wapi huko?”



    “Ni kumhusu Maxwell Ndoja. Ameapa kutoshirikiana nasi tena. Amesema inatosha kwa yale yote tuliyoyafanya. Kwa sasa anataka kufungua ukurasa mpya.”



    “Ukurasa mpya! Bloody fool!” bwana Eliakimu alifoka. “Anamaanisha nini kusema inatosha?”



    Nade akapandisha mabega yake juu.



    “Tangu lini pesa ikatosha?” Aliuliza Eliakimu. “Maxwell anataka kunipanda kichwani sasa. inabidi ajue hichi ni kitabu, hakuna ukurasa mpya kama haupo wa zamani, na ukitoa karatasi moja kwenye riwaya basi riwaya nzima inapoteza maana.”



    Aliposema hayo akaulaza mgongo wake kwenye kiti akizama fikirani. Kwa dakika kama moja kukawa kimya kabla Nade hajamuuliza:



    “Kwahiyo tunafanya nini, mkuu?”



    Bwana Eliakimu akanyaka simu yake, akatafuta jina la Max, akaliita. Baada ya muda mchache ikapokelewa.



    “Max, tunaweza tukaonana?” bwana Eliakimu aliuliza. Mzee huyu huwa haongei na mtu kwenye simu kuhusu mambo yake. Kuficha taarifa zake huwa anamwomba mtu wake wakutane. Na hupendelea zaidi nyumba yake kama mahali pa makutano.



    “Hapana, hatuwezi kukutana,” ikajibu sauti ndani ya simu.



    “Kwanini?”



    “Kwasababu sina tena sababu ya kukutana na wewe mheshimiwa. Nadhani kibaraka wako ameshakwambia.”



    “Max!”



    Simu ikakata. Bwana Eliakimu akaitazama kana kwamba haamini.



    “Amekata!” akasema akimtazama Nade. “Hivi huyu ananijua ama ananisikia?”



    Akashusha pumzi ndefu … akakuna kidevu … akakuna kichwa.



    “Hatuwezi tukamwacha huyu mtu hai,” akasema Bwana Eliakimu. “Anajua siri zetu nyingi mno. Hawezi akatoka tu kienyeji namna hii. Tutapataje uhakiki wa taarifa zetu kwake?”



    “Hilo ndiyo jambo kubwa. Siri ziko mashakani sasa. hatuwezi jua nini kimemsukuma akajitoa kwenye duara.”



    “Kwanini hukummaliza?”



    “Nisingeweza kummaliza pasipo idhini yako.”



    Eliakimu akanyanyuka akiweka mikono yake nyuma ya mgongo.



    “Hakikisha kesho unammaliza huyu punguani. Usibakize ushahidi wowote nyuma!” alisema bwana Eliakimu kwa macho ya kumaanisha.



    “Sawa, mkuu. Nitajitahidi,” Nade akapokea kauli.



    Eliakimu akaenda zake chumbani. Alikuwa amekunja uso akibinua mdomo.





    ***





    “Kwanini ulimuua Fakiri?” Jona alimuuliza Bigo aliyekuwa hapo kitini kwa masaa ya kutosha sasa. Bigo hakuwa amekula wala kunywa chochote. Tangu alipofungiwa kwenye kiti hakuwa amesogea wala kwenda popote.



    Kuepusha asije akapiga makelele na kuzua tafrani, Jona huwa anamfunga mdomo pale anapotaka kulala ama kuondoka.



    Bigo alitabasamu akimtazama Jona kwa kebehi.



    “Sijui nini unaongelea,” akajibu kisha akalaza kichwa chake kutazama chini.



    “Bigo, unapenda kuhangaika na kuteseka namna hii?” Jona aliuliza. “Mimi sina shida na wewe, najua wewe ni kibaraka tu unayetumwa. Mimi nina shida na bosi wako. Na shida yangu ni kujua kwanini anataka kuniua. Kwanini mnataka kuniua?”



    Bigo akatabasamu.



    “Ngoja nikwambie kitu kimoja, msanii. Sisi huwa hatumfuati wala kusumbuka na mtu asiye na faida kwetu, tunamfuata yule aliye na chetu, yule ambaye ana kitu tunachokitaka.”



    “Mimi nina kipi chenu?”



    Bigo akatikisa kichwa kichovu.



    “Sina haja ya kukwambia, utakuja kujua mwenyewe. Kwa sasa mimi ni wa kufa tu, aidha nifie kwako ama kwa mkuu wangu. Najua hataniacha hai. Kwahiyo sina cha kupoteza, fanya upendacho.”



    “Sina haja ya kukuua. Nipe taarifa ninazozitaka.”



    “Alafu?”



    “Nitakuacha uwe huru.”



    Bigo akajaribu kucheka, ila zoezi likashindikana. Hakukuwa na ushirikiano toka tumboni.



    “Huru? … siwezi kuwa huru kamwe maisha yangu yote.”



    “Kwanini unasema hivyo?”



    “Kwasababu najua. Njia pekee ya mimi kuwa huru ni kifo, la hasha sipo huru kabisa. Kwahiyo kama unataka kuniweka huru, inabidi uniue.”



    “Sina haja ya kukuua, Bigo.”



    “Basi mimi mwenyewe nitajiweka huru.”



    “Kivipi? – huwezi kujiua hapo.”



    Katika hali ya kushangaza, Bigo akaanza kuvuja damu nyingi mdomoni. Jona akashangazwa sana na hilo tukio. Alimkagua Bigo na macho yake lakini hakuona kama ana mushkeli popote pale.



    Mbele ya macho yake, Bigo akalegeza kichwa, akakata pumzi.



    Muda mfupi mbele, bado Jona akiwa ameduwaa, ulimi ukatoka mdomoni mwa Bigo na kudondokea chini!



    Bigo alikuwa ameunyofoa ulimi wake kwa kutumia meno!



    “Shit!” Jona akaalaani. Alishika kiuno akitafakari. Hakutaka kumuua Bigo ila bado tu msala ulimwangukia. Sasa hakuwa na namna nyingine zaidi ya kwenda kumzika, tena wakati huo huo wa usiku isije ikaleta nongwa.



    Aliubeba mwili wa Bigo mpaka uani kisha akachimba shimo na kuuzika. Zoezi hilo lilimchukua nusu saa kulimaliza. Alikuwa ametepeta jasho, akaenda kuoga kabla hajatulia sebuleni kutafakari.



    Bigo ameshaenda sasa nini anafanya? Akapata wazo la kufuatilia yale maneno ya kichina ‘pumzi ya mwisho’. Alihisi pengine inaweza kuwa ishara ikamsaidia kugundua vitu vingine muhimu na vikubwa.



    Akaunganisha tarakilishi yake na mtandao toka kwenye simu kisha akaanza kuwandawanda mtandaoni. Aliandika maneno yale ya kichina na maana yake kwa kiingereza alafu akaanza kusaka majibu.



    Baada ya punde majibu kadhaa yakaja. Akaanza kuyapitia moja baada ya moja.



    Taarifa zilikuwa finyu. Na taarifa nyingi katika hizo finyu hazikuwa zile anazozitaka. Lakini asitoke mtupu akakutana na taarifa moja, tena iliyojifichaficha huko mwishoni mwishoni.



    Taarifa hii ilikuja kabla ya kidogo hajaghairi. Ilikuwa inawahusu watu wawili huko Shanghai – China waliouawa na polisi.



    Jona akapitia taarifa ya tukio hilo ambalo lilitukia mnamo mwaka 2002. Akaja kugundua watu hao wawili walikuwa wametumwa kummaliza mfanyabiashara mmoja wa vipuri ambaye kwa bahati yake alitoa taarifa mapema kwa polisi.



    Mfanyabiashara huyo aliwaambia polisi alitumiwa ujumbe mfupi kwenye simu yake: ‘Pumzi ya mwisho’ siku moja kabla hajavamiwa. Hakuuelewa ujumbe huo ila kwa usalama wake maana ana maadui wengi kibiashara akatoa taarifa polisi.



    Hapo sasa Jona akajua kumbe ‘Pumzi ya mwisho’ ni kitu ambacho kipo ulimwenguni na si tu Tanzania pekee, ni mtandao mpana, lakini pia ni kitu cha muda mrefu. Na tageti yake kwa kiasi kikubwa ikiwa ni watu wakubwa, haswa wafanyabiashara.



    Wauaji hao wa ‘pumzi ya mwisho’ waliuawa na polisi kwenye majibizano ya risasi hivyo haikupatikana taarifa yoyote toka kwao. Haikujulikana nani aliyewatuma na ni kwa malengo gani.



    Jona aliamua kutafuta jina la mfanyabiashara huyo aliyenusurika kifo, akapata taarifa aliuawa baada ya juma moja tu tangu aliposalimika. Aliuawa kwa risasi na watu wasiojulikana waliotumia gari lililokuwa kwenye mwendokasi.



    Kumbe alikuja kutafutwa na kuuawa! Jona akatahamaki. Alitafuta na kutafuta lakini hakupata kingine zaidi ya hicho.



    Hili likamaanisha kwa Jona kwamba wauaji hawa wa ‘Pumzi ya mwisho’ walifanikiwa kutekeleza mauaji yao mengine pasipo kujulikana. Ishu ya mfanyabiashara huyu wa vipuri ilikuwa ndiyo pekee ambayo iliwaweka uchi, angalau ikaacha nyayo juu ya mchanga.



    Lakini wapo nyuma ya nani? Nani anawatuma na kwa ajili ya malengo gani? Hayo bado yalimsumbua.



    Aliona njia pekee ya kupata majibu ni kwa kutumia udadisi wake kwenye hili jambo la Fakiri. Huo ndiyo moshi pekee ambao unaweza kumwonyesha moto upo wapi.



    Akadhamiria kukutana na mjane wa Fakiri, na kama akifanikiwa basi atapata ngazi ya kumpeleka hatua nyingine.



    Akazima tarakilishi yake na kwenda kuchomoa chupa ya kileo toka kwenye jokofu. Akaenda nayo mpaka kitandani alipoketi na kunywa taratibu kilevi hicho huku akitafakari na huku akingoja kileo kimkate fikira alale.



    Baada ya kama robo saa, chupa ikawa kando wakati yeye akiwa tayari ameshajigeuzia upande mwingine.





    ***





    Majira ya saa kumi na moja na dakika kumi na nane asubuhi, Afrikana: Mbezi beach, Dar es salaam.





    “Chai ipo tayari,” alisema mwanamke mmoja mnene mweusi aliyekuwa amevalia gauni la kulalia. Makadirio ya umri wake miaka thelathini na mapema hivi. Alikuwa anamwambia mwanaume mwenye umbo la saizi ya kati, maji ya kunde, akiwa anatengenezea suruali yake akijitazama kwenye kioo.



    Kwa makadirio pia, umri wake haukuwa mbali sana na wa mwanamke, ambaye kwa wazi alikuwa mkewe.



    “Ahsante, umeshawaamsha watoto?” mwanaume akauliza.



    “Yah! Wanajiandaa saa hizi, si unajua shool bus lao linavyowahi.” mwanamke akajibu kisha akaenda kitandani alipoketi na kuendelea kumtazama mwanaume ambaye hakukaa muda mrefu sana kabla hajatoka ndani ya chumba kwenda sebuleni kupata kifungua kinywa.



    Zoezi hilo likamchukua dakika nane tu, akarejea tena chumbani kuchukua mkoba wake na kumuaga mkewe.



    “Usisahau kuja na kile kitu, sawa?” mwanamke alisema akimtazama mume machoni. Mume akatabasamu.



    “Nitaomba unikumbushe kwa ujumbe majira ya jioni.”



    “Sawa,” mwanamke akaitikia kisha akambusu mumewe kumuaga. Mwanaume akatoka ndani mpaka kwenye gari, Suzuki – vitara nyeupe, akatupia begi lake viti vya nyuma na kuwasha gari.



    Ila kabla hajasogeza chombo kwenda popote pale, ghafla akajikuta akibanwa pumzi na kitambaa. Alipapatika kwa muda mchache mno kabla hajalegea akilaza kichwa chake akiachama mdomo wazi.



    Anatoka mwanamke ndani ya gari akiwa amevalia suti nyeusi, suruali ya kitambaa na koti, mkono wake wa kuume umeshikilia pochi nyeusi. Alikuwa amevalia wigi kubwa jeusi lililokuwa linaficha uso wake.



    Alifuata uzio akaukwea na kujimwagia nje ya nyumba. Alipitia pale ambapo nyaya ya umeme zilikuwa zimekatwa.



    Haikujulikana aliingiaje kwenye gari na kufanikisha zoezi lake, hiyo kazi sasa wakaachiwa polisi wahangaike nayo.



    Mwanamke huyo aliposonga mbali na nyumba aliyofanya tukio, akatoa simu ndani ya pochi na kutuma ujumbe:



    ‘Tayari kazi imeisha.’



    Alipoona taarifa kwamba ujumbe umefika, akarejesha simu ndani ya pochi. Akapotea akiacha msiba nyuma.





    ***





    Majira ya saa kumi na nusu jioni, ndani ya nyumba ya mheshimiwa Eliakimu.





    “Naona umekuja on time!” alisema Eliakimu kwa tabasamu akipeana mkono na Miranda.



    “Si unajua ukiitwa na mheshimiwa lazima uzingatie muda,” alisema Miranda akirudisha tabasamu kwa Eliakimu.



    “Nyie ndo’ waheshimiwa wenyewe bwana, sio sisi! – karibu sana.”



    “Ahsante, nimeshakaribia.”



    Alikuja mfanyakazi wa ndani akapewa oda ya kuleta vinywaji laini. Maongezi yakaendelea baina ya Miranda na Mheshimiwa.



    “Nimekuita hapa kwa ajili ya ule mpango wetu, nataka nikupatie mrejesho wa hatua ambayo imefikia sasa.”



    “Ndio, Mheshimiwa.”



    “Kila kitu kipo sawa, mambo yameenda kama ambavyo nilitaka yaende japo kuna kamushkeli kadogo kalijiri ila nimeshakasuluhisha. Nimeshaongea na kuwapanga wahusika. Sasa kinachohitajika ili tumalize hii hatua yetu ni pesa.”



    Mfanyakazi akakatisha kidogo maongezi yao kwa ujio wake wa kuleta vinywaji – sharubati ya embe. Kila mtu akateka glasi yake moja toka kwenye trei, mfanyakazi akaenda zake, maongezi yakaendelea:



    “Hii pesa ambayo inahitajika hapa si yangu, la hasha. Ni ya kufanikisha tukio kwa kuwapatia mgao hawa vibaraka wadogowadogo angalau ili wafunge midomo yao. Kama unavyojua sisi ni waelekezaji na wasimamiaji ila utendaji upo mikononi mwao.”



    “Ndio, mheshimiwa.”



    “Sasa nawasikiliza ninyi. Hili jambo la malipo yao mtalikamilisha muda gani?”



    Miranda akanywa kwanza kinywaji fundo moja, kisha akauliza:



    “Ni kiasi gani, Mheshimiwa?”



    “Aaaah mama, kwani haufahamu? Kiasi ni kile kile cha siku zote. Kwani tulishawahi kubadili?”



    “Sawa, Mheshimiwa. Lakini siwezi kukupa majibu ya moja kwa moja pasipo kuonana na mkuu wangu kwanza. Inabidi nimfikishie hizi taarifa.”



    “Unajua kabla sijakutafuta wewe, nilimtafuta kwanza yeye maana najua yeye ndiye mhusika wa mambo ya fedha. Na nilifanya hivyo kwa siku mbili kabla sijakutafuta wewe. Hakuwa anapokea simu zangu wala kujibu meseji zangu. Sijajua nini shida.”



    “Pengine anakuwa ametingwa tu.”



    “Kiasi cha kutoweza hata kurejesha ujumbe mfupi? Na ilhali anajua kabisa kuna jambo nyeti lipo mbele yetu?”



    Miranda akakosa cha kusema.



    “Au mna mpango mwingine wa ziada?” Mheshimiwa akauliza akimtazama Miranda machoni. Miranda akahisi msisimko fulani mwilini.



    Swali hili lilifanya sharubati aliyokunywa igome kupita kooni. Alijitahidi kukaza macho yake yasizalishe shaka, akatikisa kichwa.



    “Hapana, Mheshimiwa, usiwe na mawazo hayo. Hatuna mpango wowote ule. Hili jambo la mawasiliano si kwako tu, hata kwangu pia. Kwa muda kidogo sijawasiliana na mkuu. Hapatikani kwenye simu yake … ndiyo maana nikasema pengine amebanwa na kazi.”



    “Sasa anabanwa na kazi gani kama hizi zake hazifanyi? … Anyway, hili jambo ni la haraka. Kumbukeni huu ni mpango haramu hautakiwi kuvuta muda otherwise utabumburuka.”



    “Nimekuelewa mheshimiwa. Nitajitahidi kadiri ya uwezo wangu kufanikisha hili.”



    “Kama kuna tatizo mnaweza mkanishirikisha. It’s ok.”



    “Sawa.”



    Miranda alishindwa hata kumaliza sharubati yake. Akaweka glasi chini na kuaga.



    “Mbona mapema hivyo?”



    “Kuna mahali natakiwa kupitia, Mheshimiwa.”



    Hakutaka kubakia zaidi hapo. Aliona kadiri anavyokaa hapo basi muda si mwingi anaweza akashtukiwa.



    Alipopanda gari na kutoka ndani ya jengo la Mheshimiwa akampigia simu BC na kumpasha habari aliyokumbana nayo. BC akamtaka waonane kesho yake kwani amebanwa na kazi kwa muda huo.





    ***





    Baadae kwenye vyombo vya habari na mitandaoni taarifa ya mauaji ya afisa wa serikali ajulikanaye kwa jina Maxwell Ndoja ikasambaa na kutawala.



    Picha za afisa huyo akiwa kwenye gari lake ambalo bado lilikuwa linachemsha injini, ndizo zikawa mjadala huku na huko watu wakishangazwa kwa namna tukio hilo lilivyofanyika kwa ustadi.



    Msemaji wa jeshi la polisi alisema tukio hilo lilifanyika majira ya asubuhi ya mapema ambapo mlinzi aliziraishwa na muuaji kabla hajafanikiwa kumnusisha sumu afisa huyo.



    Mke wa marehemu ndiye aliyetoa taarifa polisi ya kumkuta mumewe amekufa ndani ya gari baada ya kwenda kumtazama kutokana na kupata mashaka kuliona gari kwenye majira ya saa moja ilhali mumewe aliaga kuondoka muda mrefu nyuma.



    Hakuna uharibifu wowote uliotokea zaidi ya ukataji wa nyaya za umeme na hakuna mtuhumiwa yoyote aliyekamatwa. Upelelezi unaendelea.





    Nade na bwana Eliakimu wakatazama habari hiyo kwa tabasamu. Kazi si kwamba ilikuwa imeisha bali pia ilikuwa imetendwa vema.



    Lengo la kutazama habari hiyo ilikuwa ni kuthibitisha kama tendo limefanikiwa, yani Max amekufa, na hakuna ushahidi wowote ulioachwa nyuma.



    Hivyo vyote kwa pamoja vilikuwa vimepatikana. Bwana Eliakimu akampongeza Nade kwa kazi nzuri.



    "Hujawahi kuniangusha, Nade. Inabidi nikupe zawadi nzuri, kubwa!" Alisema kwa tabasamu.



    "Nimefanya tu kazi yangu, wala usijali mkuu," Nade akasema akitabasamu kwa haya.



    "Ndio ni kazi yako, ila umeitenda vema. Anayetenda mema siku zote hupongezwa."



    "Ahsante mkuu. "



    "Unataka zawadi gani nikupatie?"



    "Yoyote tu mkuu unayoona nastahili."



    Eliakimu akajikuna kidevu akitabasamu.



    "Sawa, najua nitakupatia zawadi gani. Nipe muda kidogo wa kuitafakari."



    Nade akatikisa kichwa kuafiki. Eliakimu akaendeleza maongezi:



    "Vipi alikupatia mushkeli kwenye tendo?"



    "Hapana. Hakuweza kufurukuta hata kidogo."



    "Kabisa?"



    "Ndio. Alipovuta hewa mara moja tu basi habari yake ikaishia hapo hapo."



    "Aisee! Hizi dawa zina nguvu eenh?"



    "Sana! Zinaonekana ni kali mno. Ile glovu niliyovaa kwa ajili ya tukio nimeitazama hivi punde nimeikuta imekatikakatika na kulainika kama bubble gum!"



    "Serious?"



    "Ndio, mkuu."



    "Unajua haya ndiyo madawa yanayosafirishwa kuingizwa nchini na wakina Miranda?"



    "Yah ulinambia."



    "Nilifanya tu kuchomoa chupa moja kwa ajili ya kaudadisi changu, nikagundua ni sumu ila sikuwa makini kwenye kuchambua madhara yake.



    Kama ni makubwa hivi, hili jambo linatisha, ni hatari. Itabidi tufuatilie kwa karibu namna mwili wa Max utakavyokuwa baada ya kuingiza sumu hii mwilini."



    "Kwenda hospitali?"



    "Hapana, mbona kuhangaika hivyo? Nitaenda tu msibani kutoa pole. Bila shaka mke wake ataeleza yote nayotaka kuyafahamu."



    Nade akatikisa kichwa kuafiki.



    "Huenda tukaja tumia pia sumu hizi kummaliza yule mtu wetu baada ya kumaliza kazi," Mheshimiwa akapendekeza na kuongezea:



    "Siku tutakayokata mzizi huo wa fitna, nitafurahi sana na roho yangu itakaa kwa amani. Hilo ndilo jambo pekee lililobakia likininyima usingizi."



    "Usijali, mkuu. Nalo litaisha," Nade akasema kwa kujiamini.



    "Siku litakapoisha, nitahakikisha, kwa uwezo wangu wote, nakutafutia zawadi ambayo hautaisahau maishani mwako daima! Umesikia?"



    "Nimesikia, mkuu."



    "Haya nenda kapumzike sasa kesho uendelee na kazi."



    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    **





    Saa mbili asubuhi maeneo ya Masaki, Dar es salaam.



    "Karibu!" Sauti ya kiume ilifoka tokea ndani ya uzio, punde geti likafunguliwa na kichwa kikachomoza kutazama nje.



    Alikuwa mwanaume mweusi mwenye nywele ndogo pilipili. Amevalia koti kubwa rangi ya bluu na suruali ya kitambaa miguuni akiwa peku.



    Alivyotazama nje akakutana na Jona aliyekuwa amevalia shati jeupe la drafti, suruali ya kitambaa na mokasi nyeusi.



    "Naweza nikakusaidia?"



    "Ndio, bila shaka hapa ni kwa marehemu Fakiri."





    Mwanaume getini akatikisa kichwa kukubali.



    "Mimi ni afisa polisi," Jona akaonyeshea kitambulisho chake bandia. "Nimekuja hapa kuonana na mwenye nyumba."





    "Kuna tatizo gani afande?" Mwanaume getini akauliza upesi. Macho yake yalibeba hofu.



    "Hamna tatizo," Jona akamshusha presha.

    "Ni kwamba nahitaji tu kufanya naye maongezi."



    "Kuhusu marehemu au kuna jipya?"



    Jona hakujibu, akamkazia macho mwanaume huyo.



    "Karibu, unaweza ukaingia tu."



    Jona akazama ndani mpaka sebuleni. Mke wa marehemu Fakiri akaitwa kuja kuungana naye.



    Alikuwa mwanamke mnene mfupi maji ya kunde. Alivalia dera la njano lenye maua mekundu mekundu.



    Macho yake yalikuwa madogo, mashavu makubwa na kidevu kisichoonekana.



    Alimkarimu Jona kwa sauti nyembamba ya chini.



    "Unatumia kinywaji gani?"



    "Hapana, mama, nashukuru wala usijichoshe. Nipo sawa."



    "Hata chai?"



    "Hapana,mama. Basi naomba unipatie maji ya kunywa kama hutojali."



    Mama akamwita mwanaume yule aliyempokea Jona, Sabi kwa jina, akamwagiza alete maji ya kunywa.



    Jona akajitambulisha na kueleza dhamira yake. Alikuwa hapo kwa lengo la kufufua kesi ya bwana Fakiri iliyopotelea hewani.



    "Kuna taarifa chache nazihitaji toka kwako," akasema Jona. "Naomba ushirikiano wako kamilifu."



    "Usijali, lakini sina taarifa yoyote mpya. Zote nilishatoa kwenu polisi."





    "Utaniambia tu hizo hizo ambazo ulizitoa. Kama nilivyosema hapo awali, tunaifufua hii kesi."



    "Karibu."



    Mama huyu hakuonekana mtu mwenye matumaini. Si bure alichoshwa na mahojiano ya aina hiyo, hakuona jipya ama la maana.



    Alikuwa anatimiza tu wajibu.



    "Kuna adui yoyote wa kibiashara unayemhisi pengine anahusika na mauaji ya mumeo?"



    "Hapana."



    "Hamna yeyote?"



    "Ndio."



    "Wewe unahisi kwanini mumeo aliuawa?"



    "Sijui. Siku zote ukiwa na mafanikio, maadui hawakosekani."



    "Mama, nipo hapa kwa ajili ya kusaidia. Najua umechoshwa na mahojiano ya aina hii na pengine waona yanakupotezea muda.



    Tafadhali, naomba unipe ushirikiano wako. Nakuahidi utaona matunda ya hichi utakachokifanya," Jona alisema kwa kujiamini akimtazama Mama machoni.



    Muda mfupi macho ya mama yakawa mekundu.



    "Nimeongea na kuongea sana, nimelia na kusaga meno lakini hakuna aliyejali. Alipotokea mtu wa kujali, naye hakuishi wakammaliza!"



    Mama akajipangusa machozi kwa vidole vyake.



    "Pole mama, najua inaumiza. Nitafanya kadiri ya uwezo wangu kuwaleta wahusika wote mbele ya haki."



    Mama akawa kimya kwa muda kidogo. Ni kama vile alikuwa anavuta kumbukumbu, ila iliyokuwa inamchoma, uso wake ulijieleza kwa ndita za majonzi.



    "Nakumbuka kabla mume wangu hajafa, alikuwa ananiambia kila usiku maisha yake yapo mashakani. Nilimuuliza kwanini haendi polisi, akawa ananijibu haitosaidia.



    Sikumwelewa anamaanisha nini mpaka pale alipokuja kufariki. Ile kauli yake ya haitosaidia kweli nikaanza kuishuhudia."



    "Alikuwa anakwambia nini kinaweka maisha yake rehani?"



    "Ndio. Unajua alikamatwa kwa kosa la kutokulipa kodi. Bishara yake ikayumba sana kwa maana ilikuwa ni kiasi kikubwa sana alichotakiwa kulipa, mbali na msongo wa mawazo.



    Akahangaika huku na huko kutafuta pesa hiyo lakini hakuipata kwa wakati.



    Alipokuja kupata haikuwa kamili, bali nusu ya ile anayotakiwa kulipa. Alinambia amepewa na mshirika mmoja wa kibiashara anayeitwa Sheng.



    Lakini pesa hiyo alipewa kwa masharti ambayo alishindwa kuyatimiza na hatimaye kuuawa."



    "Naomba uniweke wazi kila kitu mama. Masharti gani hayo? Na huyo Sheng wamjua?"



    Mama akafuta kwanza machozi kabla hajasema:



    "Hakuniweka wazi, alinambia kifupi tu kuwa ameambiwa asafirishe vitu fulani ndani ya mzigo wake wa samaki kwenda Rwanda na Burundi."



    "Na huyo Sheng?"



    "Simjui. Yeye mwenyewe mume wangu hakuwa anamjua. Sheng ni mtu wa kutuma watu tu. Walikuwa wanakuja hapa wawakilishi wake kuteta na mume wangu."



    "Kwahiyo ina maana mumeo aligoma kusafirisha mzigo huo?"



    "Ndio. Hivyo Sheng hakumalizia kumpatia nusu ya pesa anayodaiwa mpaka kiasi fulani cha mzigo kitakaposafirishwa.



    Sasa mume wangu baada ya kupata nusu ile toka kwa Sheng, akaamua kutafuta nusu nyingine ambayo kwakuwa kiasi kilikuwa kishapunguzwa, akaipata kwa urahisi.



    Kabla hajalipa, wakamuua."



    Mama akamalizia kwa kulia. Ikabidi Jona apoteze kama dakika nne kumbembeleza kurudia kwenye hali ya kuongea.



    "Na kumhusu mwanao? Kifo chake kinahusiana na haya?"



    "Ndio. Salim alikuwa anataka kutafuta haki ya baba yake. Unajua Salim alikuwa anashirikiana sana na baba yake kwenye mambo ya biashara. Alikuwa anajua mengi huko kuliko mimi.



    Shida yake ilikuwa ni kutafuta haki ya baba yake, ila matokeo yake akapata kifo."



    Jona alinakili yale yote aliyopata kwa mama huyo. Alipomaliza akamuaga na kumpa moyo. Alimwambia:



    "Haki itapatikana, hata kama yakawia."





    ***





    Saa nne usiku: Lorenzo Night club.



    Baada ya kugongesha glasi zilizojazwa mvinyo, Lee akanywa fundo moja kubwa kisha akauliza wenzake watatu waliokuwa pamoja naye mezani.



    "Bado kimya?"



    Wakatazamana kwanza. Wengine hao watatu walikuwa ni Nigaa, Devi na Mombo; kampani yake ya kazi.



    Wote walikuwa wamevalia jeans za bluu zilizokuwa zinatofautia kukoza. Juu wakivalia matisheti, isipokuwa Lee peke yake ambaye alivalia jaketi dogo jeusi mtindo wa kizibao.



    "Naona bado kimya," akajibu Mombo na sauti yake nzito baada ya wenzake kuwa kimya kujibu swali.



    "Usikute Bigo kamalizwa na sisi tupo hapa tunabung'aa?" Akasema Devi. Sauti yake muda wote ilikuwa inakwaruza kama bati linalosuguliwa na msumari.



    "Home kwake hayupo, wala maskani zake. Muda sasa hajatutafuta. Si kawaida!" Nigaa naye akatia neno kisha kukawa kimya.



    "Kwa namna bosi anavyomtafuta, akimpata anaweza akamtafuna mbichi," Devi akasema akitikisa kichwa chake kama mtu anayesikitika.



    "Ila mimi nina mashaka," akasema Lee. "Bigo atakuwa yupo matatizoni. Akili yangu inagoma kabisa kuamini kama yu buheri wa afya."



    "Sasa tutafanyaje?" Akauliza Mombo. Na hilo ndilo lilikuwa la msingi, watafanyaje kama wanatilia mashaka juu ya Bigo?



    "Nina wazo," akasema Nigaa. "Kwanini tusiende kumuuliza mkuu juu ya yule mshkaji ambaye alitakiwa kuuawa na Bigo?"



    "Ili?" Devi akauliza.



    "Ili tumfuatilie mshkaji wetu. Kama jamaa huyo aliyetakiwa kuuawa bado yupo hai, maana yake Bigo ndiyo atakuwa ameuawa."



    Kukawa kimya kidogo watu wakimeza wazo hilo.



    "Naunga mkono hoja," Lee akasema akitikisa kichwa. "Kama kweli tunataka kujua hatma ya Bigo, hiyo ndiyo njia pekee."



    Basi wakakubaliana wote kufanya vivyo.





    "Vipi kama Bigo atakuwa ameuawa?" Akauliza Mombo.



    "Sasa kutakuwa na kingine zaidi ya kummaliza huyo aliyemuua?" Akatahamaki Nigaa. "Ni kumuua tu na yeye, moja kulipiza kisasi cha msh'kaji wetu. Na mbili kumaliza kazi ambayo Bigo atakuwa ameishindwa."



    Wakaendelea kunywa. Na baadae wakawaita wanawake kwa mujibu wa idadi yao waendelee kufurahia.



    Wakadumu hapo mpaka kwenye majira ya saa tisa usiku, kisha kila mmoja akaelekea upande wake.



    Lee akiwa ameongozana na mwanamke mrefu mwembamba mwenye nywele ndefu za bandia wao wakaenda hotelini.



    Hoteli kubwa yenye jina la TUMID, hapo wakachukua vyumba na kujiweka ndani.



    Wakaenda kuoga kisha wakarejea ndani.



    "Naomba pesa yangu kwanza," akasema mwanamke akisugulisha vidole vyake.



    "Shilingi ngapi?"



    "Laki moja!"



    "Mbona kubwa?"



    "Ndiyo bei ya kulala na mimi usiku mzima."



    "Usiku mzima na saa hizi ni saa tisa?"



    "Kwani si usiku? Na si nitaondoka asubuhi?"



    Lee asibishane, akakubali. Ila akilini mwake alikuwa ameshapanga kumdhulumu mwanamke huyo kwa kumpatia pesa ile anayoona anastahili.



    Unajua hawa wanawake wakiona ngozi nyeupe huwa wanawehuka na kudhani wana pesa, aliwaza Lee. Ila nitamkomesha, akaweka nadhiri.



    Wakapeana penzi kabla Lee hajachukuliwa na usingizi mzito uliompeleka mpaka asubuhi ya saa moja.



    Alifungua jicho moja akaangaza, hakukuwa na mtu kitandani. Haraka akakurupuka na kukagua chumba kizima. Hamna mtu.



    Akaenda na bafuni napo, hakuona mtu pia.



    Akili yake ikamtaka atizame suruali yake upesi. Akatazama na kukagua mifukoni, mifuko yote ilikuwa meupe!



    Hakubakiziwa hata mchanga.



    Akalaumu sana. Badala ya kukasirika akajikuta anatabasamu, na mwishowe akacheka. Alijiona fala kabisa, tena yule mtepetevu.



    Aliketi juu ya kitanda akashika kichwa akiuchambua usiku mzima namna ulivyokuwa. Akahisi tumbo limekuwa la baridi punde alipokumbuka kuwa ndani ya suruali aliweka pochi.



    Macho yakamtoka, mdomo ukamkauka.



    Pochi ile ilikuwa na vitu vya msingi na maana sana. Ilikuwa na nyaraka zake za siri! Ni bora mwanamke yule angekomba pesa akamwachia vinginevyo.



    Akanyanyuka na kushika kiuno. Tumbo lilinguruma. Alihisi miguu inapoteza nguvu.



    Alikuwa amefanya uzembe mkubwa sana ambao hata kuwaeleza marafiki zake ilikuwa ni aibu. Ni kwa namna gani hilo liliwezekana wakati yeye huwa mwangalifu?



    Akahisi ametiliwa madawa. Hilo ndilo jibu pekee ambalo lilionekana kusuuza nafsi yake japo hakujuwa ametiliwaje madawa hayo.



    Sasa alipata kibarua ambacho hakukitarajia- kibarua cha dharura. Cha kumtafuta mwanamke huyo ampatie pochi yake kulinda nyaraka zilizomo ndani.



    Hakuwaza pesa. Lah! Aliwaza nyaraka. Alijikuta anamiminika kijasho chembamba akipepesa pepesa macho chumba kizima kana kwamba kaambiwa na mshenga pochi ipo ndani.



    Alihofia endapo pochi hiyo ikikamatwa na mikono isiyo salama. Itakuaje?



    Kwani ni nyaraka zipi hizo zi ndani ya pochi?



    ---



    "Huwezi amini, leo nimeangukiwa na embe chini ya mwarobaini!" Alisema mwanamke ambaye ndiye yule aliyemzidi kete bwana Lee.



    Hapa alikuwa na mwenzake mfupi mnene ndani ya chumba kimoja kikubwa kipana kilichotandikwa godoro chini.



    Chumba hichi kilikuwa kimejazwa vitu lukuki chini mathalan chupa ya chai na beseni dogo jekundu lililokuwa limesheheni vyombo.



    Hakukuwa na vitu vingi humo. Na hata vilivyokuwepo havikuwa vya thamani kubwa, wala havikuwa vimepangiliwa vizuri.



    Ila ukiwatazama wanawake hawa walivyokuwa wameupara. Loh! Waweza sema makazi yao ni Abu dhabi. Nywele feki za bei, na nguo ambazo si haba.



    "Enhe! Nipe mchapo!" Akadakia mwanamke mwingine kwa mdomo wake mpana.



    "Bwana wee si nimekutana na mchina si mchina, mjapani si mjapani, sijui mkorea yule jana kule golini."



    "Nilikuona mwenzangu. Nikasema la haulaa! Ushaula shoga maana mie mwenzako nilitoka kapa."



    "Yaani nimeula nimeula! Ila mama mchina mwenyewe anatwanga Kiswahili kama kazaliwa Kigogo!"



    Wakaangua kicheko.



    "Kwahiyo hakuwa na pesa?"



    "Nawe wapenda kuwahi mbele, tuliaa."



    "Haya nafunga bakuli."



    "Pesa alikuwa nazo ila akajifanya anabania. Nikasema hunijui wewe. Chap! Nikafanya mambo yangu yale. Kaingia kichwa kichwa chali! Nikajibebea vyangu."



    "Shing'ngapi?"



    "Najua basii? Nimefungua pochi hivi, naona madola dola tu."



    "Weee!"



    "Oooh! Nakwambia hivyo."



    Mwanamke yule mwivi akatoa pochi ya Lee toka kwenye mkoba wake akamkabidhi mwenziwe ambaye aliidaka na kuifungua haraka.



    Hakukuta kitu!



    "Mbona sioni kitu?" Akauliza akiendelea kukagua.



    "Nimekuonyesha ushahidi tu, pesa nishazitoa."



    "Na wewe bana! Na hivi je?"



    "Hivyo vitambulisho vitambulisho vyake. Mie sijahangaika navyo!"



    "Sasa si bora ungemwachia tu. Umevibeba vya nini?"



    "Hivi we unadhani nilipata muda wa kukagua kagua pochi? Mie nilifunua nikaona pesa, basi nikaitupia tu mkobani."



    Yule mwanamke aliyebebelea pochi akatazama na kukagua vitambulisho na karatasi zingine alizokumbana nazo huko.



    Alitazama kwa muda kabla hajaamua kuachana nazo kwa maana hakuwa anaelewa.

    "Naona yameandikwa kwa kichina china na Kiingereza tu."



    Akatupia pochi kando na kuanza kujadili namna watakavyotumbua pesa iliyopatikana.



    Laiti kama wangelikuwa wanalijua namna Lee anavyotoka jasho kuitafuta hiyo pochi, wangemrudishia hata kwa kumtuma wakala.



    ---



    "Can I see you?"(Naweza kukuona?) Jona aliuchapa ujumbe huo kwenye simu yake kisha akautuma. Alikuwa ndani ya mtandao wa Facebook akichati na mke wake Eliakimu.



    Ni majira ya jioni haya na siku hiyo Jona hakwenda popote pale zaidi ya kuhama toka chumbani kwenda sebuleni, sebuleni chumbani siku nzima.



    Alichokifanya punde tu alipoamka ni kumtaarifu Jumanne kwamba hatakuja kazini kisha akalala kwa muda kidogo kabla hajaja kuamka jua likiwa tayari limeshanawiri.



    Alipika akala, akateka tarakilishi yake na kuanza kurandaranda mtandaoni. Alianzia huko Facebook ambapo hakupata anachokitaka. Akatoka na kwenda kwenye mambo mengine.



    Muda huu sasa ndiyo anarejea baada ya kuona mtu anayemtaka yupo hewani.



    "See me? Serious?" (Kuniona? Kweli?) Uliuliza ujumbe wa Miriam, mke wa Eliakimu.



    "Yes for sure!" (Ndio kabisa!) Akachapa Jona na kutuma.



    "How can you see me while you are so far?" (Unawezaje kuniona ingali upo mbali?)



    "I am in Nairobi now for a fashion show." (Nipo Nairobi sasa kwa ajili ya onyesho la mitindo.)



    "Nairobi???"



    "Yes. You don't believe? - I am in Nairobi and I expect to be in Dar es salaam soon." (Ndio. Huamini? - nipo Nairobi na nategemea kuwa Dar es salaam karibuni.)



    "Sure, I would love to see you." (Kweli, ningependa kukuona.)



    "Me as well. Hope to you see soon. Bye!" (Mimi pia. Natumai kukuona karibuni. Kwaheri!)



    Jona akaaga na tabasamu. Mbinu yake ilikuwa inaendelea kutimia. Hakutaka kujirahisisha kwa 'mteja' wake huyo ili kutompatia doa la shaka.



    Alitaka Miriam apate picha kwamba yeye ni mtu ambaye yupo bize, ametingwa na kazi. Ana muda mchache sana wa kuteta na watu mitandaoni.



    Alipotoka kwenye mtandao huo wa Facebook, akazima kabisa tarakilishi yake alafu akajiandaa kwa muda mfupi kabla hajatoka ndani akibebelea tarakilishi.



    Akaenda internet café, sehemu wanapofanya biashara ya mtandao, akakutana na mhudumu: mwanamke mmoja mweupe, akamuulizia kuhusu huduma ya scanning.



    "Ipo," akajibu mhudumu pasipo kumtazama Jona. Alikuwa yupo bize kutazama tarakilishi yake akichezesha vidole kwenye keyboard.



    Jona akatafuta mahali pa kukaa. Punde akaja mhudumu kumsikiliza. Akampatia kibahasha cheupe.



    "Humo kuna picha, naomba uziskani na kuzituma kwenye hii kompyuta."



    Mhudumu akatikisa kichwa kisha akaenda. Jona akawasha tarakilishi na baada ya mfupi akaona picha zile zikiwa zimetumwa.



    Mhudumu akaja kuulizia muda wa mteja na pesa yake. Jona akalipia kisha akaendelea na shughuli zake.



    Akafungua injini ya kusaka majibu alafu akaanza kuchukua picha moja baada ya nyingine na kuanza kuzisakia majibu yake mtandaoni.



    Alifanya hivyo kwa picha zote hizo kasoro ya Fakiri. Akajikuta amepata majibu ya picha mbili tu zingine zikiwa hazina mrejesho wowote wa maana.



    Picha ya kwanza ilikuwa ni ya mwanaume mwalimu wa shule ya sekondari ya Lamu, Thadeus Malima, na ya pili ni ya aliyekuwa mbunge wa jimbo la Nyamagana, Mwanza, kwa jina Ditto Jigeleka.



    Wote hawa walikuwa wameuawa kwa risasi. Na muuaji akiwa bado anaitwa 'asiyejulikana'. Mauaji ya watu hawa yalitenganishwa na masaa matano tu.



    Hapo Jona akapata shaka kidogo juu ya mtendaji wa mauaji haya. Huyu mwalimu alikuwa ni wa shule iliyopo Dar es salaam, wakati mbunge akiwa ni wa Mwanza.



    Muuaji alitekelezaje mauaji haya kwa tofauti ya masaa matano tu?



    Hata kama alipanda ndege, bado ikamuwia vigumu kuamini kwani mauaji haya yalihitaji mipango thabiti.



    Kwahiyo kuna muuaji zaidi ya mmoja? Na wote wanakuwa na hizi picha?



    Kabla hajasumbuka sana na hayo maswali akaendelea kuperuzi juu ya marehemu mbunge maana yeye ndiye ambaye taarifa zake zilikuwa zinapatikana kwa wingi ukilinganisha na bwana Thadeus ambaye mtandao ulimtambua kwa taarifa za kifo tu na akaunti ya Facebook.



    Akiwa anapekua pekua kuhusu taarifa hizo, akagundua kwamba mauaji ya Jigeleka yalikuwa yalikuwa yanahusishwa na sababu za kisiasa kwakuwa alikuwa chama pinzani akianzisha hoja iliyoonekana kuibana serikali huko bungeni.



    Lakini Jona alikuwa mwerevu kung'amua jambo. Muuaji alikuwa ana mipango na malengo fulani. Ukitazama kwa Fakiri na kwa huyu mbunge, utapata kugundua muuaji alikuwa anacheza na matukio na hivyo basi kuacha watu njia panda kwa kusingizia jambo fulani.



    Haswa serikali.



    Alimaliza muda wake wa kuperuzi akajirudisha nyumbani. Lakini hakuwa amepoteza muda wala pesa kwani kuna kitu alikuwa amepata. Ila basi alitokea kujiuliza sana kuhusu picha ya yule mtu mmoja ambaye hakuwa amepata taarifa zake miongoni mwa zile picha.



    Ina maana yeye hajauawa au taarifa zake hazijulikani? Alitamani kujua ili kama basi hajauawa aweze kumwokoa, ila akajikuta hana cha kufanya. Hana pa kuanzia kupata hizo taarifa.



    Akiwa anawaza waza na kujiuliza, akakumbuka kuna kitu alitakiwa kupitia kwenye tarakilishi yake. Mojawapo ya faili moja ambalo alilikomba toka kwenye simu ya marehemu Bigo.



    Basi haraka akavuta mashine hiyo na kwenda kwenye faili alilolitunza kwa jina la ‘Bigo docs’ akafungua na kwendea faili moja kando ya kioo likiitwa ‘gallery’. Humo akakuta picha nyingi sana.



    Hakuona hasara kupitia picha moja baada ya nyingine.



    Miongoni mwa picha hizo nyingi zilikuwa zikimwonyesha Bigo akiwa sehemu mbalimbali na watu mbalimbali.



    Jona alivutiwa na picha kama tano hivi ambazo alipata kuzitenga kadiri alivyokuwa anazitazama. Picha tatu zilikuwa zinamwonyesha Bigo akiwa na marafiki zake: Lee na wenza. Na mbili zingine akiwa na mwanamke fulani hivi na watoto ambao Jona alihisi wanaweza kuwa familia ya Bigo.



    Akazitazama picha hizo kwa umakini. Mojawapo akagundua mandhari yake kutokana na uwenyeji wake ndani ya jiji. Picha hii ilikuwa imepigwa Mango garden, Bigo akiwa na marafiki zake.



    Hizo zingine kidogo ikawa ngumu kutambua wapi zilipigwa. Akaziweka kapuni.



    Lilikuwa ni swala la muda tu. alijua atapata kujua kadiri hatua zitakavyosonga mbele. Acha apumzike kwanza.





    ***





    Usiku wa saa tatu, ndani ya nyumba ya BC.



    Miranda akiwa amevalia suruali ya jeans rangi bluu, na tisheti nyeupe. BC alikuwa amevalia suti ya udongo pasipo kuweka kikolombwezo kingine chochote zaidi ya saa kwenye mkono uliokuwa umebebelea sigara kubwa.



    Mezani kuna chupa kubwa ya champagne na glasi mbili.



    “The guy might sense something fishy,” (Jamaa huenda akahisi jambo mrama.) alisema Miranda akimtazama BC. “You know he’s in this dirty game for long. He has that nose to smell when things turn awkward.” (Unajua yupo kwenye huu mchezo kwa muda mrefu. Ana pua ya kumfanya anuse pale mambo yanapoenda kombo.)



    Miranda alikuwa anahofia. Kwa namna ambavyo Eliakimu alikuwa anamtazama mara yake ya mwisho wakiongea naye, kulimfanya ahisi jambo fulani halipo sawa.



    Hakuwa anamchukulia Eliakimu kiwepesi hata kidogo.



    “Have you told him about his price being high?” (Umemwambia kuhusu bei yake kuwa juu?) BC akauliza.



    “That’s of you to tell him.” (Hilo ni lako kumwambia.) Akajibu Rhoda kabla hajanywa kinywaji chake. Jibu hilo likaonekana ni kali kwa mkuu. BC alisafisha koo lake lake asitie neno. Akanyanyua glasi ya kinywaji na kunywa.



    Walikuwa njia panda haswa. Walihitaji muda zaidi wa kumsubirisha Eliakimu, ila hilo jambo likaonekana ni gumu kutokea.



    Miranda aliona hamna njia nyingine bali kukubali tu kuhusu Eliakimu kwani kuhusu upande huu mwingine wa Boka na mkewe, wanaofuatilia hauwezi kuzaa matunda kwa wepesi hivyo.



    Kidogo hilo likawa gumu kwa BC kulipokea. Alijaribu kulisindikiza na kinywaji lishuke ila bado likang’ang’ania koo.



    “Wait, I shall talk to him seriously this time and address him about our offer. It’s up for him to decide either to dig in or out. I don’t mind waiting but loss.” (Ngoja, nitaongea naye kuhusu hili swala kwa umakini muda huu na kumwambia kuhusu ofa yetu. Ni juu yake sasa kukubali aidha kuwa ndani ama nje. Sijali kungojea bali hasara.)



    Ungeona sura ya Miranda, haikuwa sawa. Alipuuza akanywa glasi mbili za kinywaji kwa pupa kabla hajanyanyuka na kuaga, kuna kazi inamngojea nyumbani.



    Alitoka akaenda kwenye makazi ya Kinoo, wakateta kwa kama dakika tatu kabla hawajaachana.



    ---



    Asubuhi ya saa kumi na moja, Miranda akadamka akajitia kwenye gari lake kuanza safari mpaka maeneo ya Makumbusho, si mbali sana na kituo cha mabasi. Hapo akapaki mahali anapostahili na kutulia ndani ya gari akiangaza.



    Punde akawaona watu kadhaa wakiingia ndani ya jengo. Akangojea mpaka majira ya saa mbili ndipo akashuka na kuzama ndani ya jengo.



    Jengo hilo lilikuwa limebebelea bango kubwa likisomeka: ROADAR SOLAR COMPANY. Pembeni ya bango hilo kulikuwa kuna mabango mengine ya ofisi zingine zilizokuwa zinapatikana ndani ya jengo hilo.



    Miranda aliekea kwenye ofisi hii ya solar – umeme wa jua, akaomba kuonana na mkurugenzi wa kampuni. Pasipo kuzungushwa, akapewa nafasi hiyo. Aliingia ndani ya ofisi akamkuta mwanaume mmoja mnene mweusi mwenye kiwaraza.



    Alikaribishwa kwa ukarimu akaketi na kueleza shida yake ni kuunganishiwa umeme wa jua kwenye jengo lake zima, jengo kubwa la biashara.



    “Huduma hiyo inatolewa,” akajibu mkurugenzi. “Kwani haujapewa maelekezo huko ulipotoka?”



    “Nimepewa, sema nikaona ni uwekezaji mkubwa na hivyo natakiwa kuongea nawe. Nahitaji mradi huo utekelezeke sio tu kwenye ofisi zangu hapa bali pia na huko mikoani.”



    Wakaongea kwa muda wa dakika kumi na tano kisha wakaagana.



    Lengo la Miranda halikuwa biashara bali upelelezi. Macho yake yalikuwa yanatambaa tambaa huku na huko kukagua na kuchambua. Mpaka anaondoka alikuwa ameshapata anachokitaka.



    Aliwasiliana na Kinoo wakakutana na kumpasha habari.



    “Ile kampuni ya umeme wa jua, ni ya wale wachina.”



    “Umejuaje?”



    “Nimeona mojawapo ya picha ya mkuu wao ukutani.”



    “Kweli?”



    “Ndio, ni kampuni mtoto ya wale wachina.”



    Kinoo akatikisa kichwa. Sasa alikuwa ameshaunganisha dots za uthibitisho, ya kwamba aliyemuua Bite ni wachina, mahasimu wao. Ndiyo hao wanaoitafuta ile picha. Picha ambayo na wao wanaitaka.



    Picha ambayo wanaamini wakiipata itakuwa ndiyo mwanzo wa wao kuwamaliza mahasimu hao. Walitokea kuamini picha hiyo ina ujumbe. Ina neno ambalo Bite alitaka kulisema.



    Bite hakuwepo katika upande wowote ule: aidha wa wachina ama wakina Miranda. Daraja hili lilikuwa muhimu. Haswa kwa wakina Miranda ambao wanaamini kwa kiasi kidogo ambacho Bite alikuwa na wale wachina, basi kuna kitu alivuna.



    Wakakubalia na Miranda kwamba inabidi baadae wakaonane na Jona. Tena wote kwa pamoja.



    “Inabidi ajue kwamba yupo hatarini,” alisema Miranda. “Kama alifanikiwa kumkamata moja wa memba wao, basi inabidi ajue yupo kwenye orodha na hawataacha kumfuata.”





    ***





    Saa mbili usiku, Lorenzo Night club.





    Lee alitoka kwenye gari, Noah ya kijivu yenye vioo vyeusi, akanyookea moja kwa moja ndani. Bado muda haukuwa umeanza kuiva ndani ya eneo hili hivyo hakukuwa na watu wengi. Hata hao aliowakuta ni kwasababu tu ilikuwa ni mwisho wa wiki.



    Klabu hii ni ya usiku, si usiku wa saa mbili kama huu, bali usiku mzito.



    Lee alitembea klabu nzima akipekua mazingira kwa macho yake madogo. Mashaka yalikuwa yameshika uso wake kana kwamba mpangaji aliyepoteza ufunguo pekee uliobakia.



    Aliongea na mlinzi wa eneo hilo akijaribu kumfafanulia umbo la mwanamke yule aliyemkwapulia vitu na kumuuliza kama amemwona eneoni hapo. Mlinzi akatikisa kichwa. Hakumwona.



    “Tafadhali ukimwona, naomba umshikilie na unipashe habari,” alisema Lee akimkabidhi mlinzi namba yake ya simu na shilingi elfu kumi. “Ukifanya hivyo n’takupatia zaidi.”



    Alifanya hivyo kwa watu watatu kabla hajatoka ndani ya klabu na kurudi ndani ya gari. Ndani alikuwepo Nigaa akiwa amekaa pembeni ya kiti cha dereva ambacho ndicho Lee alikalia.



    “Umempata?” Nigaa akauliza.



    “Hapana,” Lee akajibu akitikisa kichwa.



    “Nilikwambia, ila ukashindwa kuelewa. Huu siyo muda wao. Tatizo lako una haraka mno.”



    “Siwezi nikangoja zaidi,” Lee akajibu. Alikuwa amechanganyikiwa.



    “Brother, huna haja ya kuhofia. Yule malaya atakuja tu hapa na tutampata kiurahisi. Ulikuwa huna hata haja ya kupoteza pesa yako.”



    Wakangoja na masaa yakazidi kwenda mpaka saa saba usiku, mwanamke yule hakuonekana. Saa nane … saa tisa, kimya.



    “Imekula kwetu,” Nigaa akasema.



    “Sasa nafanyaje?” Lee akauliza.



    “Inaonekana hili zoezi litatuchukua zaidi ya leo hii.”



    Walikaa hapo mpaka kwenye mishale ya kukaribia asubuhi pasipo kumwona mtu wanayemngoja. Waliamua kutia moto chombo na kwenda zao. Lee akiwa na mawazo na majuto.





    Akitafakari na kudadavua kichwani. Akitanabahi ni njia gani ya kuenenda pasipo kupata majibu yoyote yale. Aliwaza endapo mkuu wake akipata habari hizi, nini kitatokea.

    Hakuna kingine zaidi ya kifo.





    “Nigaa, naomba ushike usukani,” alisema Lee akiegesha gari pembeni. “Sijisikii vema.”





    “Usiwaze sana, Lee. Huyo malaya tutampata tu,” Nigaa alimpa Lee moyo.

    “Shida si kumpata, Nigaa. Bali yale yaliyomo mule kwenye pochi kama yatakuwepo salama. Sijawahi kufanya uzembe wa aina hii.”





    Nigaa alichukua usukani wakaendelea na safari mpaka kwenye makazi yao ambapo waliamua kupumzika kwanza kabla ya baadae kuendelea na kazi zingine. Haswa ya kwenda kuonana na mkuu wao awaeleze kumhusu mtu yule ambaye Bigo alitumwa akammalize.





    Kwenye majira ya saa nane mchana wakawa tayari wameshaamka na kujumuika na mwenzao aitwaye Mombo wakaenda kuonana na mkuu wao.





    Wakamweleza haja ya mioyo yao. Mkuu akawataka watulie kwani tayari hilo jambo ashalichukulia hatua.







    “Wo yijing fale lìng yigè rén,” (Tayari nimeshamtuma mtu mwingine,) alisema mkuu akikuna kidevu chake chongofu. “Ràng women kàn kàn hui fasheng shènme.” (Acha tuone nini kitatokea.)

    Kwahiyo hapo wakawa hawana tena kauli mpaka pale yule aliyetumwa arejeshe taarifa ama naye atokomee ndipo mkuu achukue hatua nzito.





    Kwasababu Jona ni mchoraji tu, hamna haja ya kuhofia sana mpaka kutuma kikosi kamili.



    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mwanaume aliyetumwa alijulikana kwa jina la Panky. Mwanaume fulani mwembamba urefu saizi ya kati. Kichwani mwake alikuwa ana nywele zilizochongwa kama mtaro zikiwa zimesimama kama moja.





    Kwa shingo upande Lee na wenzake wakaridhia. Ila kabla hawajaondoka, mkuu akauliza:





    “Lee, ni hái hao ma?” (Lee, upo sawa?) Akimtazama Lee machoni. upesi Lee akatazama chini na kutikisa kichwa chake kuridhia ya kwamba alikuwa sawa. Wakatoka nje.









    ***







    Saa nane mchana …







    “Vipi upo poa now?”

    “Ndiyo, nadhani nina muda sasa. Tunaweza tukaenda.”

    “Saa hii?”

    “Ndio. Au wewe ulikuwa unataka twenda muda gani?”

    “Usiku. Bila shaka ndiyo muda atakaokuwa nyumbani.”

    “Unajua usiku nina miadi na Boka. Siwezi kwenda, kama unavyojua kuna ishu nataka nichonge naye.”

    “Lakini sidhani kama muda huu atakuwepo nyumbani. Mchana huu.”

    “Basi fanya hivi, si upo town, pitia pale ofisini kwake umcheki.”

    “Nipe kama robo saa.”

    “Iwe kweli.

    Baada ya robo saa …

    “Hayupo!”

    “Pamefungwa?”

    “Hapana. Yupo yupo mshkaji mwingine.”

    “Muulize basi.”





    Punde, Kinoo anashuka kwenye gari na kufuata ofisi ya Jona. Alimkuta Jumanne pekee ambaye alimsalimu na kumuulizia Jona.





    “Atakuwa yupo kwake, jana na leo hajafika job. Ila naweza nikakusaidia.”

    “Usijali,” akajibu Kinoo. “Nilikuwa namhitaji yeye mwenyewe.”





    Akarudi kwenye gari na kumtumia Miranda ujumbe:





    “Tuelekee nyumbani.”

    “Poa, nipitie nipo tayari,” ujumbe ukajibu.





    ____







    Saa nane na dakika hamsini na tano …







    Jona alikuwa amevalia bukta na kaushi nyeupe. Kuna baadhi ya michoro alikuwa anaiweka sawa kwenye ubao wake wa karatasi, michoro ambayo kwa kuitazama upesi huwezi jua alikuwa anachora nini hasa.





    Alisikia hodi getini, akaacha shughuli yake na kuangaza dirishani. Akaona Range Rover sport nyeupe. Akashtuka kidogo. Alijua usafiri huo ni wakina nani. Basi akaenda chumbani na kukwapua bunduki yake aliyofichia nyuma ya kiuno akiijaladia na shati jeusi.





    Kwa kujiamini akalifuata geti na kuwaruhusu wageni waingie ndani.

    “Hatujaja kwa shari, bali maongezi,” alisema Miranda. Mwanamke ndani ya sketi fupi nyeusi na topu ya pinki. Akiongozana na Kinoo mwenye nguo zijulikanazo kila uchwao.





    Jona akawakaribisha sebuleni akiketi kwenye kiti cha kando kilichoruhusu kila mmoja kumtazama mwenzake.





    “Karibuni japo ujio wenu haukuwa na taarifa. Natumai mlikuwa mnajua kama nipo nyumbani.”



    “Ndio, tulipitia kazini kwako.”

    Pasipo kupoteza muda Miranda akaeleza kilichowaleta. Ya kwamba ni picha na baadhi ya taarifa ambazo wanataka kumfikishia Jona.





    Wakamwambia kuhusu msako ule wa picha, haswa wakiuhusisha na kundi la kihalifu la kichina ambalo lipo nyuma yake. Ya kwamba picha ile ni mali yao, wanaitafuta na kwa gharama yoyote ile wataipata.





    “Uhai wako upo hatarini. Watu hawa hawatakoma kutuma watu wao mpaka pale watakapohakikisha wameitia hiyo picha mkononi. Japokuwa hatujawahi kuiona hiyo picha, tunaamini itakuwa na nyaraka muhimu sana kwao. Na ndiyo maana nasi twaisaka.”





    Huu ukawa muda muafaka kwa Jona kuuganisha tarifa zake kichwani na kupata mantiki. Ina maana wageni wake hawa wanawafahamu hawa wachina ambao alikuwa anahangaika kufumbua fumbo?





    Hawa wachina ambao wamefanya mauaji ya watu kadhaa!





    Kabla hajaongelea picha, akawauliza wakina Miranda kama wanafahamu lolote juu ya kifo cha bwana Fakiri na Jigeleka. Wakasema hawafahamu. Jona akawaambia ni kwa namna gani amepata taarifa za hao marehemu.





    “Nilikuta picha zao kwenye hifadhi ya mtumishi wao.”



    “Bila shaka walikuwa kwenye pumzi zao za mwisho,” akasema Miranda. Jona akakumbuka neno hilo ‘pumzi ya mwisho’. Ni neno la kichina lililoandikwa kwenye picha za watu wale aliowaona kwenye paspot.





    “Unajua lolote kuhusu pumzi ya mwisho?” Akauliza.



    “Ndio, najua. Ni kikosi cha mauaji kinachohusika na mauaji ya wale wote wanaoleta kizingiti mbele ya kazi yao. Kikosi hichi kinaundwa na watu stadi wa kazi. Wenye uwezo wa kuua pasipo kubakiza ushahidi wala kielelezo.”



    “Na unajua kilichomuua bwana Jigeleka?”



    “Hapana, sijajua. Wanaua watu wengi, siwezi nikajua haswa kwanini kila mmoja huuawa.”





    Baada ya Jona kuuliza maswali ya kutosha, akataka kujua kwa undani juu ya wakina Miranda, wao ni wa kina nani haswa na wanajishughulisha na nini. Miranda akajibu kwa ufupi kwamba wao ni wafanyabiashara, wakihusika na biashara za kuingiza madawa nchini, madawa ya afya wakiwa na ubia na MSD.

    “Makajuanaje na hawa wachina?” Jona akauliza.





    “Kwasababu walikuwa ndiyo wapinzani wetu kibiasara. Siku zote rafiki huwa karibu, ila adui karibu zaidi.”



    “Sasa picha itawasaidia nini?”



    “Kama tulivyosema ni adui zetu. Tunataka kujua kila nyendo yao.”



    “Basi?”



    “Basi. Hicho pekee ndicho kinatuhusu.”





    Jona akakereketwa rohoni. Kwanini watu hawa wanafanya uhalifu nab ado wanadunda mtaani? Kwanini wanaua watu nab ado hawachukuliwi hatua? Alijaribu kuwauliza wakina Miranda, akajibiwa kwa ufupi.





    “Mikono na miguu yao ina mafunzo. Akili zao zina ujuzi. Mifuko yao ina pesa.”





    Wakateta kwa ufupi kabla Jona hajaenda kuwaletea picha ambayo aliwakabidhi na kuwaambia:



    “Mnaweza mkanishrikisha kama kuna jambo mtaling’amua kwenye picha hiyo. samahani sitawapa mwende nayo.”

    Miranda na Kinoo wakaridhia.



    Wakaitazama picha kwa umakini sana wakila dakika kama kumi na tano. Lakini wakatoka patupu!





    “Una uhakika picha yenyewe ni hii?” akauliza Kinoo.



    “Ndiyo yenyewe. Sina zaidi.”





    Mbona ni picha ya kawaida tu? visiwa na ndege! Wakatahamaki. Hawakujua nini haswa dhamira ya picha ile. Waliona ni kama urembo.





    Ila kama isingelikuwa na maana kwanini itafutwe? Kwanini Jona alengwe kuuawa?





    “Hamna chochote ulichokipata pichani?” Miranda akamuuliza Jona. Jona akatikisa kichwa.





    “Hapana. Nikadhani pengine nyie mwajua.”





    Wote walitota. Hakuna aliyeona cha maana. Ila Jona akasisitizia lazima picha hiyo itakuwa na maana, hawana budi kufuatilia.





    “Nakumbuka wakati Bite ananiambia nimchoree hii picha alinipa maelezo very simple, ila alitaka niyafuate na kuyazingatia haswa. Nilirudia kuchora picha hii mara tatu, tena kwasababu ndogo ndogo sana, mara ndege wamekaa mbali, niwasogeze, ama visiwa ni virefu sana na kadhalika. Bila shaka alikuwa na maana yake.”





    Mwishowe Jona akawakabidhi wakina Miranda picha nyingine, kopi ya ile orijino ambayo aliichora kwa penseli na karatasi, wakakubaliana yeye abakie na ile orijino.





    “Jona,” Miranda akaita. “Wewe ni nani?” Akauliza. Jona akatabasamu kwanza kabla ya kujibu kwa kuuliza:

    “Kwanini wauliza?”

    “Kwasababu wewe si mchoraji pekee. Wewe ni nani?”

    Jona hakutaka kusema mambo mengi, akawaambia hayo mengine yatakuja kadiri na muda.

    “Kuwa makini sana,” Miranda akamsisitizia Jona.

    “Usijali,” Jona akamjibu. “Naweza kujitazama vema.”







    _____







    Robo saa mbele...







    "Mkuu, kuna jambo lipo katikati ya Jona na na wakina Miranda,"Nade akatoa taarifa. Wakati huo alikuwa amejiweka kando kidogo ya nyumba ya Jona macho yake ndani ya miwani yakiwa yanaangaza kutazama gari, Range Rover sport nyeupe, ikiishilia.





    "Ndio, nimewaona wakiingia ndani ya nyumba ya Jona," akasema Nade sasa akianza kuchukua hatua kusonga mbali na nyumba ya Joana.





    "Wametoka muda si mrefu. Wamedumu kwa muda wa kasoro lisaa."





    Akasikilizia kidogo, kisha akasema:

    "Sawa, mkuu. Ila inakuwa ngumu kujua wanachokiongelea. Nahofu isije ikawa ni kuhusu Miriam."





    Kimya kidogo akisikilizia. Kisha akasema:

    "Sawa, mkuu. Jicho halitafunga."

    Akakata simu. Ila mara akasikia mkono wa mtu begani. Haraka akageuka.

    Kutazama alikuwa ni Jona!

    .



    Nade alishtuka, ila kumeza mshtuko huo akatabasamu kana kwamba hakuna kilichotokea. Akamtazama Jona na macho ya wenza, akiuliza:



    “Kuna tatizo?”



    Jona akatikisa kichwa kukataa. Lakini akamtaka Nade wakapate maongezi kidogo ndani kama hatojali. Nada akatazama kwanza saa yake kabla hajabinua mdomo na kupandisha mabega.



    “Ts ok!”



    Wakati wanageuka, mara Nade akaona gari fulani kwa mbele yao. Haikuwa umbeli mrefu sana na gari hili lilikuwa limewapa ubapa.



    Lilikuwa ni Altezza moja nyeusi, vioo vyake vyote vilikuwa vimezibwa isipokuwa cha dereva pekee.



    Kufumba na kufumbua, dereva huyo akatoa mkono wenye bunduki ambayo mdomowe aliuelekezea kule alipo Nade na Jona. Nade akatoa macho kwa mshangao. Katika kasi ya ajabu, akamsukuma Jona waangukie chini.



    Sauti ya risasi ikavuma, paah!



    Risasi ikatoboa bega la Nade, na mara gari ikachomoka mbio kupotea. Jona akamkarimu Nade kwa kubana mkono wake kwenye jeraha. Huku akimwambia kwamba wana haja ya kumuona daktari haraka iwezekanavyo.



    “Sitaki kwenda hospitali,” Nade akasema.



    Basi Jona akambeba begani na kwenda naye mpaka nyumbani. Akamlaza chini na kisha akaleta pamba na kopo kubwa la spirit. Kisha akaleta na vifaa fulani ambavyo Nade alistaajabu Jona amevitolea wapi.



    Akagundua kwamba ndani ya nyumba ya Nade kulikuwa kuna vitu karibia vyote. Wakati Nade anahangaika kumtibia, yeye alikuwa anapekua pekua, japokuwa hakuona kila jambo, alifanikiwa kuona angalau vichache.



    Jona akatoa chuma cha risasi begani mwa Nade, na kisha akampakaa spirit.



    “Upo tayari nikushone.”



    “Ndio,” Nade akajibu.



    Jibu hilo likamshangaza sana Jona maana hakulitegemea kama lingetoka hivyo haraka tena pasipo kusita. Hapo akajua namna gani mwanamke huyo alivyo jasiri. Alivyo mgumu na roho ya kijeshi.



    Kuthibitisha hilo zaidi, Jona akachukua uzi na kumshona Nade. Nyuzi si chini ya tano zikaenda begani. Nade akiwa ameng’ata kipande cha mti ambacho Jona alikuwa amemkabidhi apate kupotezea maumivu.



    “Ulijifunzia wapi haya?” Nade akauliza.



    “Sehemu mbalimbali tu. Nilikuwa napenda sana kuwa daktari ningali mtoto.”



    Wakamaliza zoezi lao na kuketi. Jona akamhudumia Nade pombe kali kwenye glasi kisha maongezi mafupi yakachukua nafasi.



    “Umekuwa ukinifuatilia toka muda gani?” Jona akauliza. Nade akajitahidi kukanusha ila mwishowe akakubali kwamba alikuwa anamfuatilia Jona kisiri kwa mujibu wa amri ya mheshimiwa Eliakimu.



    “Unajua anakuwa na presha kama kazi yake itafanyika au lah.”



    Sababu hiyo ikagoma kuiingia ndani ya kichwa cha Jona. Akauliza:



    “Nade, Eliakimu anamhitaji mkewe kwasababu gani haswa? Kuna nini ambacho hataki nigundue?”



    Nade akakanusha yote hayo akimsisitizia Jona kwamba wao shida yao ni Miriam tu. na hapohapo akaulizia harakati za Jona kumtafuta mwanamke huyo zimeishia wapi.



    “Bado naendelea, msijali nitawataarifu.”



    Maongezi hayo hayakudumu muda mrefu kwasababu kila upande ulikuwa mwangalifu kupitiliza kutamka lolote. Mwishowe wakajikuta wanajadili mengine ambayo yalionekana kusisimua kila upande.



    “Ilikuaje ukakutana na Eliakimu?”



    Nade akashusha kwanza pumzi. Akasema hapendi kuongelea sana mambo yake ya kale. Ila basi kwakuwa ametaka kujua, hana budi kumjuza.



    Watu wengi wamekuwa wakiamini kwamba Nade ni ndugu yake Eliakimu kwa uaminifu wake na uchapakazi wake. Lakini pia kujitolea kwake kumfanyia kazi mheshimiwa huyo, ila kiuhalisia ni kinyume.



    “Mimi nilikuwa mfanyakazi wa ndani wa bwana Eliakimu. Tokea kipindi hicho akiwa anagombea ubunge tu na hana hili wala lile kuhusu uwaziri. Alinitoa kwetu Tanga, kwa wazazi wangu maskini.



    Akanilelea kama mtoto wake, nikishiriki naye meza moja … si kama mfanyakazi, bali kama mwanafamilia mwenzao.”



    “Ikawaje mpaka kukupa nafasi hii?” Jona akakatiza kuuliza. Nade akatabasamu. Alijua fika huko ndipo ambapo Jona alikuwa anapataka.



    “Ni siku moja tu ndiyo ambayo mambo yalibadilika. Siku hiyo nakumbuka ilikuwa ni jumapili jioni, mheshimiwa akiwa ameshatoka huko bungeni, alifanikiwa kuupata ubunge.



    Siku hiyo alipoingia ndani, kumbe kulikuwa kuna mtu alikuwa amepanga kumuua, na mtu huyo hakuwa mwingine isipokuwa bodyguard wake. Kwa kutumia bunduki. Na alitaka kummaliza ndani ya nyumba yake.



    Kama Mungu, wakati nipo jikoni, kwa kupitia kioo cha dirisha la sehemu ya kulia chakula, nikaona bodyguard akichomoa bunduki kiunoni. Basi haraka nikanyaka birika la chai, nikatoka na kulirusha, likamkita bodyguard na kumlaza chali.



    Mheshimiwa akfurahi sana kwa kumwokoa maisha. Tangu hapo hakuamini bodyguard, na akataka mimi ndiye niwe bodyguard wake, kwahiyo akamwita mtu na kuanza kunifunda martial arts.”



    Jona akamuuliza kama walijua kwanini Mheshimiwa alilengwa kuuawa, Nade akamwambia ulikuwa ni upinzani wa kisiasa tu. Hamna cha ziada.



    Ila Nade kabla hajaondoka, akataka kujua kwanini mtu yule ndani ya gari alikuwa anataka kummaliza Jona. Kufupisha habari, Jona akamwambia hafahamu. Ila kichwani kwake tayari alishajua, si wengine bali wale wachina wanaodai picha.



    Na aliapa kuwashikisha adabu.





    ***





    “Nakuja, nakuja!” sauti ya Mudy ilisikika kwa ndanii. Nje ya nyumba yake, mlangoni alikuwa amesimama mwanaume mmoja aliyevalia suti na kubebelea mkoba wa rangi ya kahawia.



    Kutazama usoni, hakuwa mwingine bali Brokoli. Nywele zake alikuwa amezifumisha vema kuficha uzee. Macho yake alikuwa ameyavesha miwani mepesi ya jua.



    Punde mlango unafunguliwa, na Mudy anatokea akiwa ameshikilia kipande cha mkate mkononi. Amevalia bukta nyeusi ya mpira. Akatoa macho kumwona Brokoli mbele yake.



    Yalikuwa ni majira ya saa kumi hivi, ila iliyoelemewa na dakika kuifuata saa kumi na moja.



    “Mkuu!” Mudy akastaajabu na mkate wake mdomoni. “Karibu, karibu.”



    Brokoli akatabasamu akiingia. Akaketi kabla Mudy hajamuuliza angependelea kitu gani. Brokoli akasema maji tu yanamtosha. Na pasipo kupoteza muda, akasema nini kimemleta pale.



    “Kuna nyaraka fulani sizioni kule ofisini. Zipo wapi?”



    Kauli hiyo ikashtua moyo wa Mudy. Alijikuta anasisimkwa vinyweleo na kupigwa bumbuwazi.



    “Hakuna nyaraka ambazo nimechukua mkuu!”



    “Sijasema kwamba umechukua, nimeuliza zipo wapi.”



    “Sijajua. Ni nyaraka gani hizo unazoziongelea?”



    Naye Brokoli hakusema ni nyaraka hizo anazoziongelea. Basi akafungua mkoba wake na kutoa bunduki yenye kiwamba cha kumezea sauti. Akaikoki bunduki hiyo na kumwonyeshea Mudy pasipo kusema kitu.



    Mudy akaanza kuropoka. Ya kwamba nyaraka hizo amempatia Kinoo kwani alikuwa anazihitaji, na pia amepanga kuchuku hatua kuhusu kifo cha Bite.



    Brokoli akatikisa kichwa na kusema:



    “Ahsante. Hicho ndicho nilikuwa nataka.” Kisha akaminya kitufe cha bunduki, bunduki ikakohoa na kumwangusha Mudy chini. Paji lake la uso lilikuwa limetobolewa likivujisha damu.



    Brokoli akasafisha bunduki yake vema na kitambaa alichokitoa ndani ya mkoba alafu akarejesha bunduki yake mkobani baada ya kuhakikisha amebebea simu ya Mudy.



    Akatoka ndani ya uzio, na kujiweka kwenye gari lake VX ya grey, akatimka akiweka simu sikioni.



    Punde simu ikapokelewa, akasema:



    “Ameuza taarifa … kwa jamaa yule jamaa, Kinoo.” Akakata simu na kuendelea na safari.







    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog