Search This Blog

Monday 24 October 2022

NI ZAMU YAKO KUFA - 2

 

    Simulizi : Ni Zamu Yako Kufa

    Sehemu Ya Pili (2)









    Hivi sasa Ofisi Fukuzi tumeamuliwa na Rais kufanya msako wa watu hao. Polisi wataendelea na uchunguzi wao, ila kama ujuavyo kuwa hiki ni kitengo cha siri sana, hivyo kazi yetu itakuwa huru na siri kama siku zote. Jacob, nataka uende Arusha ukawatafute watu hawa. Kwa kuzingatia muda uliobaki kabla ya mkutano na kasi ya mauaji inayofanywa na watu hao, inahitajika mtu atakayefanya kazi kwa kasi na usahihi mkubwa. Najua unaweza kuwa bado hujapumzika vizuri tangu kwisha kwa ile kazi ambayo ulipambana na Kiroboto, maana ni miezi miwili tu imepita. Lakini nimeangalia nani wa kumpa kazi hii hapa ofisini, nimeona ni lazima mara hii tena nikupeleke Arusha ukatatue suala hili. Ukweli ni kuwa kazi hii inaweza kuwa ya hatari kuliko zote ulizowahi kukutana nazo, kwani hatujui ukweli kuhusu watu hao. Sina hakika kama kweli lengo lao ni kufanya majaribio ya silaha zao tu na si vinginevyo. Hivyo kukutuma wewe ni kama kukupeleka kwa adui ambaye kwa hakika hajulikani undani wake. Lazima ujue kuwa Ofisi fukuzi inakupenda na inakutegemea sana kwa hivyo ningependa ukafanye kazi hii kwa hadhali kubwa.

    Si wengi wanaojua kuwa utaelekea Arusha, ninapenda iwe kimya kimya kwani mpaka sasa hatujui adui yetu ni nani. Hivyo kazi yako ni kuhakikisha unaweza kulifikia kundi hili na kulitowesha kabla halijadhuru wananchi wengi zaidi na kuharibu mkutano muhimu kama huu tunaoutarajia ufanyike huko Arusha.

    Sitapenda kukupangia namna ya kuondoka wala kuishi kule Arusha, ila naomba iwe siri kubwa. Hii ni kwa usalama wako na wa Ofisi Fukuzi kwa ujumla.

    Utapitia gharani kuchukua vifaa unavyodhani utavihitaji katika safari hii. Lakini napenda kukueleza kuwa kuna mtu nimemwandaa kule Arusha ambaye atajitambulisha na utamtambua tu. Yeye ataweza kuwa msaada kwako pindi mambo yakiwa magumu.

    Sina mengi ya kukueleza, ila uwe makini, nakutakia kila la heri. Naamini nitapata taarifa kuwa wale watu tayari wako mikononi mwako. Jacob nakuamini na Ofisi Fukuzi inakutegemea” Alimaliza Bi. Anita huku akimpa mkono Jacob

    “Asante bosi ila naomba uzidi kuniombea kwani nahisi kila dalili ya hatari ikiwa mbele yangu” Jacob alisema huku akiwa tayari kwa kuondoka.

    “Bila shaka Jacob Mungu yuko upande wetu, upande wa haki na watetea wanyonge kama sisi” Hayo yalikuwa ni maneno ya mwisho ya mkurugenzi wa Ofisi Fukuzi Bi. Anita kwa kijana wake mpelelezi Jacob Matata.



    * * *

    Alipotoka ofisini kwa Bi. Anita, Jacob alikwenda kilipo chumba cha ofisi yake ndani ya ofisi hizo. Humo alipanga vizuri makablasha yake yaliyokuwa katika mpangilio usiovutia, kisha alikiendea kikasha chake cha siri na kukichukua. Humo alichukua zana kadhaa za kazi na kukirudisha mahali pake.

    Baadaye alielekea kwenye kiti na kukaa huku mikono yake ikiwa imepakata kichwa chake. Macho yake yakielekea darini, alikaa hivyo kwa takribani dakika kumi na ushee hivi. Alipokuwa amemaliza kufikiri aliyokuwa anafikiria alisimama na kuweka mikono mfukoni, kabla hata hajapiga hatua moja mara simu yake ya kiganjani iliita. Aliiangalia kama paka aliyeona nyoka akipita. Mtazamo huo ulikuwa wa kiudadisi.

    “Nani na nikusaidie nini? Jacob Aliuliza katika sauti yake ya simba.

    “Mzee Edson Kinyaro”

    Mara moja Jacob alimkumbuka. Huyu mzee ndiye aliyemuokota mtaani na kumtaka akasomee mambo haya ya upelelezi.

    “…ni hivi bwana Jacob, kuna mauaji ya kushangaza yanatokea hapa Arusha. Jana usiku aliuawa moja wa majaji wa mahakama ya kimataifa ya Arusha. Jana asubuhi wameuwa watu kadhaa pale Hospitali ya mkoa ya Arusha. Tangu hapo wameshauwawa askari wapatao kumi na mmoja akiwemo, Inspeka wa Polisi Sogoyo.

    Kinachoumiza kichwa zaidi ni kuwa zimebaki siku chache ili mkutano huu muhimu wa viongozi wa ukanda huu wa Afrika ufanyike hapa Arusha. Lakini kwa tetesi nilizo nazo ni kwamba mkutano huo upo matatani kufanyika kwa sababu kuu mbili. Kwanza, kuna barua za vitisho ambazo zimesambazwa na watu wasiojulikana zinatoa vitisho juu ya mkutano huo. Katika taarifa yao hiyo ya vitisho, watu au kundi hilo lisilojulikana limesema kuwa litafanya kitu ambacho kitaacha wazi mdomo wa kila atakayesikia lile watakalolifanya kwa viongozi hao waliopanga kukutana Arusha. Kufuatia barua hizo za vitisho, viongozi wa vikundi na serikali wameanza kutangaza kutohudhulia mkutano huo kwa sababu za kiusalama.

    Hebu fikiria kijana wangu jinsi haya mambo yanavyofanyika, inauma sana pale wengine wanapojaribu kujenga na wakati huohuo wengine wanakazana kubomoa na kuharibu. Haijulikani watu hao ni watu gani, wana nia gani na wako chini ya nani. Asante bwana Jacob kwa kunisikiliza, nina imani hutanyamaza na hata kama ukinyamaza, usijali sana nitakuwa nakutaarifu kila mauaji na ubaya utakaokuwa unafanyika”. Alipotaka kukataa simu ndipo Jacob kwa hasira akamwuliza

    “Tafadhali, hivi hukuona mtu mwingine wa kumwambia taarifa hizi?

    “Wengi nimewaona na nawafahamu, lakini nimeichunguza mikono yao na kutambua kuwa hawangepokea taarifa hizi katika mtazamo na hali ninayotaka waipokee” Alijibu mzee huyo kama mtu aliyekuwa amelitegemea swali kama hilo.

    “Bado sijaelewa ni kwa nini umeamua kuniambia mimi wakati kama ni vijana wa nchi wapo wengi sana na ungeweza kuwaambia”

    “Bwana Jacob sikusita kukueleza hasa pale nilipokumbuka kuwa wakati serikali inataka kukupeleka kusomea namna ya kutatua masuala kama haya, mimi ndiye niliyetia sahini kuidhinisha fungu la kulipia gharama za mafunzo hayo”

    “Sasa mzee Edson, unataka kuniambia kuwa kati ya wote tulioenda kusomae mambo haya umeniona mimi tu?
    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Bwana Jacob kumbuka kuwa mlikuwa wengi lakini hamkuhitimu sawa. Kama mlihitimu basi hamkurudi na misimamo sawa. Wengi waliporudi toka kwenye mafunzo, tayari walishakuwa ni vibaraka wa watu fulani wa nchi hizo. Hata kama wapo waliorudi na msimamo kama wako lakini kiutendaji hamko sawa kwani wengine wameshavutwa na nguvu ya pesa. Kumbuka Jacob, haitakuwa na maana pale tutakapokuwa tunatamba kuwa ndani ya nchi yetu tuna mmoja wa wapelelezi wazuri duniani wakati hatupati huduma yake. Najua unajua kuwa kuna kosa la kiufundi lilifanyika miaka ile baada ya Pacha wako wanne kutoweka. Hatukuchukua hatua ya kusafisha. Hao ndiyo wanaosumbua kwa sasa. Nashukuru kuwa ulifanikiwa kumuondoa Kiroboto, ila safari hii kwa mujibu wa taarifa nilizo nazo, Max ndiyo yuko kazini…ameshaacha alama yake ya Sungura aliyefumba macho kila sehemu yalipofanyika mauji….”

    “Unamaanisha Max, yule Max “the Fuse”?!!!? Jacob alihamaki.

    “Yes, the Fuse himself, yuko ndani ya Arusha, anawasha na kuzima umeme anavyotaka. Jacob mwanangu, siku zote naamini kosa la kiufundi husahihishwa na fundi. Miye kama fundi mstaafu nimeshaliona kosa la kiufundi, ninahitaji fundi alisahihishe, hivyo basi inabidi ufanye kitu, maana kama ujuavyo, Max - the fuse ana uwezo ambao Polisi wa kawaida kamwe hawawezi kumkabili.

    Hata hivyo naomba unisamehe kwani sikupiga simu ili kukushurutisha kuacha mipango yako na kuja kutatua jambo hili. Najua umechoka na unahitaji mapumziko kutokana na kazi yako ngumu, hasa ile ya HEKA HEKA. Kwa heri subiri taarifa nilizokuahidi” Mzee Edson Kinyaro alipomaliza tu alikata simu. Bila shaka hakupenda maswali zaidi toka kwa Jacob.



    * * *

    Wakati Jacob Matata akiwa bado anatafakari taarifa aliyopewa na Edson Kinyaro, huku mkono wa kushoto ukiwa bado umeshikilia simu yake ya kiganjani, huyu yeye alikuwa akipewa mkono wa pongezi na bosi wake. Huyu si mwingine ila ni Max, Max “the Fuse”. Yeye ndiye aliyeteuliwa na vigogo wa mpango wa kuhakikisha mali iliyopo ukanda wa maziwa makuu inaingia mikononi mwa watu wachache. Mpango huu ulikuwa umesukwa na wazungu wachache waliopo katika nchi za magharibi.

    Kwa mtazamo wa wazungu hawa walibaini endapo watafika wao wenyewe kuendesha kampeni hii ingewawia vigumu. Hivyo wakaamua kutafuta waafrika wachache wenye sifa wanazozihitaji na kuwakabidhi kazi hii. Kazi ya kuwasafishia njia na kuwawezesha wao kuchukua utajiri uliopo ndani ya eneo la maziwa makuu bila bughuza.

    Kazi ya kwanza aliyokuwa amepewa Max ni kuhakikisha anawamaliza wapelelezi wote mashuhuri katika ukanda huu wa maziwa makuu. Kazi hii peke yake ingemwingizia pesa nyingi toka kwa tajiri wake. Pili ingekuwa kuwafyeka viongozi wote ambao wangeonekana kuwa kikwazo katika kufanikiwa kwa mipango ya wazungu hao.

    Ni katika kutekeleza kazi ya kwanza, ya kuwamaliza wapelelezi wote mashuhuri katika ukanda huu, ndipo mpango wa propaganda za silaha hatari ulipobuniwa. Hii ilikuwa na lengo la kuhakikisha kuwa wapelelezi wote mashuhuri katika Afrika mashariki watumwe kwenda Arusha ili kwenda kutafuta ukweli juu ya tetesi hizo.

    Max kwa ustadi mkubwa alifanikiwa kuingiza vijana wake hatari ndani ya Nchi, huku kwa makusudi makubwa akivujisha taarifa juu ya kuingia kwao hapa nchini.



    ha taarifa juu ya kuingia kwao hapa nchini.

    Yeye na kundi lake walipofika Arusha walitafuta namna ya kufanya mauaji ya kutisha ili kuvifanya vichwa vya viongozi wa usalama viamini kuwa kulikuwa na mabaya yaliyokuwa yanakwenda kufanyika Arusha. Kwa utaalamu wa hali ya juu walifanikiwa kwenda hospitali ya umma mkoani na kufanya mauaji ambayo yamesababisha viongozi mbalimbali wa nchi hizi kutuma wapelelezi wao huko Arusha. Jacob toka Ofisi Fukuzi ni mmoja wao.

    Hivyo wakati Jacob akiwa ofisini kwake muda mfupi tu mara baada ya kuwa amekabidhiwa kazi na bosi wake, Bi. Anita, ni wakati huo huo ambapo Max alikuwa ndani ya moja ya hoteli ya kifahari ndani ya jiji la Nairobi. Max alikuwa ameingia Nairobi kwa ndege ya asubuhi sana tokea Arusha ambako alikuwa amewaacha wenzie wakiwa wanapumzika na kufuatilia nyendo na mawasilino yoyote yaliyokuwa yakiingia na kutoka katika simu ya Edson Kinyaro.

    Nairobi alikuwa anakutana na mzungu mmoja ambaye alikuwa amekuja kwa niaba ya wenzake. Yeye alikuwa amemwita Max ili kumkabidhi orodha na picha za wapelelezi ambao wazungu hao walitaka Max na kundi lake wawamalize.

    “Naamini kazi yenu ya kuingia Arusha haikuwa ngumu sana. Na nina imani kwamba mmefanikiwa kuvifanya vyombo vya usalama kuwa na taarifa juu ya ujio wenu, kwani taarifa ya kutolewa vitisho kwa ule mkutano wa Amani ya Afrika Mashariki pale Arusha hata mimi nimezipata. Niliposikia hivyo nikajua kazi imeiva Tanzania.

    Sikiliza Max, hizi hapa ni picha za wapelelezi ambao tungependa kusikia taarifa za vifo vyao. Ukiwamaliza hawa utakuwa umemaliza kazi yako katika hatua ya kwanza. Hapo utapokea kiasi cha pesa kama tulivyokubaliana katika mkataba wetu” Alisema mzungu huyo katika lugha ya kiingereza.

    “Sawa, hesabu hii kazi imeshaisha. Jiandae kusikia vilio vikitokea huko Arusha” Alijigamba Max pasipo kujali chochote. Tamaa ya pesa ilikuwa imemjaa, mpaka kope zake zilionyesha hivyo.



    * * *

    Saa mbili asubuhi siku iliyofuata, yaani tarehe 18 Julai, 2009 ilimkuta Max akiwa tayari ndani ya Arusha. Tayari alikuwa ameshatoa vivuli vya kutosha vya zile picha alizokuwa amepewa na mmoja wa bosi wake kule Nairobi.

    Wakati huu Max alikuwa ni mwenyekiti wa kikao kilichojumuisha vijana wake wa kazi.

    “Kama mjuavyo kuwa kazi yetu ndiyo inatarajia kuanza leo hii. Bila shaka mara baada ya kusikia yote yale tuliyoyafanya pale hospitali ya mkoa na kwa yule jaji wa mahakama ya kimataifa, viongozi wengi wa usalama wa nchi hizi watakuwa wameshatuma wapelelezi wao wanaowategemea. Sasa, hapa nina picha za wapelelezi wote wanaotakiwa kuuawa. Nitawapa ninyi picha hizi halafu mtawapa vijana wetu.

    Naomba mzingatie jambo moja, hapa tunakwenda kupambana na wapelelezi wanaotegemewa na nchi zao katika ukanda huu. Ni watu wenye mbinu zote za kipelelezi na ujasusi, hivyo yeyote atakayefanya mchezo nitammaliza hata kabla hajafikiwa na wapelelezi hao. Hili ni vema mkawaambia hata vijana wengine ili wawe makini” Max aliongea katika sauti ya utulivu kana kwamba alikuwa anaongoza ibada iliyojaa watakatifu.

    Kikao hiki kiliwajumuisha watu ambao ni wataalamu watupu. Max kwa kutambua ugumu wa kazi aliyokuwa nayo alikuwa amechagua watu ambao kweli ni watu waliostahili kazi hii. Kiasi cha pesa alichokuwa amehidiwa kupewa kilitosheleza kabisa kuwalipa wataalamu hawa wa kutumia silaha na kupigana.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kwa wakati huu tutatawanyika na kwenda sehemu tulizopangiana, naomba kusiwe na makosa yoyote” Alipoongea maneno hayo wote walipiga makofi kuonyesha ushirikiano na umoja.

    Ilikuwa ni saa nne kamili asubuhi ambapo kikao hicho kilifungwa na wote wakatawanyika.



    * * *

    Nusu saa baadaye baada ya kwisha kwa kikao cha Max na wenzie, ilimkuta mpelelezi Jacob Matata tayari akiwa miongoni mwa wasafiri waliokuwa wakisubiri muda wa safari katika kiwanja cha kimataifa cha ndege cha J.K.Nyerere zamani DIA, Dar es salaam. Alikuwa tayari kwa safari ya kutoka Dar kwenda Arusha. Moyoni alijua kuwa anaenda kama mpiganaji aliyetumwa na watanzania wote wapenda amani. Pia hakupinga wazo kuwa safari hii ilimaanisha kupata au kukosa, kuua au kuuawa.



    * * *

    Mchana wa siku hiyo ulimkuta tayari ameshaingia Arusha. Kuingia kwake alipanga akufanye siri. Hakupenda mtu yeyote ajue yuko wapi na anafanya nini. Hivyo alipotelemka tu toka ndani ya ndege alitembea taratibu huku akichunguza kama kulikuwa na macho yaliyokuwa yakimfuatilia.

    Alikuwa amevaa miwani maalumu ya kijasusi ambayo humwezesha aliyeivaa kuweza kuona mbali sana. Miwani hii pia ina uwezo wa kuona mtu yeyote aliye na madhala kwa aliyeivaa. Ni miwani ya ajabu!

    Alienda sehemu moja waliyokuwa wakiuza chakula na kuagiza kahawa. Yote hii ni katika hali ya kujipa nafasi ya kuweza kuona kama kulikuwa na mtu aliyekuwa akitarajia ujio wake. Alikunywa taratibu huku macho yake yakichunguza kila mtu katika sehemu hii ya uwanja wa ndege. Mpaka alipomaliza kinywaji chake hakuwa ameona yeyota wa kutilia mashaka.

    Dakika chache baadaye zilimkuta amesimama kando ya taxi moja ya rangi ya bluu.

    ”Mzee naomba unipeleke Mlimani Hotel tafadhali” Alisema hivyo wakati tayari akiwa ameshakaa ndani ya gari. Dereva huyu aliyeonekana kuwa ni mtu wa makamo hakujibu kitu na badala yake aliwasha gari na kuliondoa kwa mwendo wa wastani.

    Baridi ya wastani na ukungu mwepesi vilikuwa vimeipamba Arusha na kuifanya iwe katika hali yake ya asili. Waliposhika barabara ya Nyerere ndipo mpelelezi Jacob Matata akapata wazo la kuangalia kama kulikuwa na gari iliyokuwa inawafuatilia nyuma. Wakati wanafika mkabala na benki ya NBC tawi la Arusha ambalo liko jirani na Maktaba ya vitabu ya mkoa wa Arusha, upande wa mbele wa Polisi mesi, ndipo alipopata uhakika kuwa kulikuwa na gari lililokuwa likiwafuatilia.

    Alitabasamu. Alifurahi kugundua kuwa kuna wajanja kama hao. Wakati bado anafikiria juu ya nani ambaye alikuwa amejua juu ya kuwasili kwake na kuamua kumfuatilia, jambo jingine lilimshangaza. Kilichomshangaza ni uamuzi wa dereva kuamua kuacha kuelekea Mlimani hoteli ambayo iko jirani na makutano ya barabara ya kijenge, Njiro, Philips na hii inayotokea mjini, badala yake dereva huyo akashika njia nyingine. Alipomtupia macho dereva huyo mshangao uliongezeka kwa Jacob baada ya kuonana na tabasamu alilokuwa usoni mwa dereva huyo.

    Akiwa bado anashangaa tabasamu hilo na kujaribu kutafsiri kuwa lilikuwa limebeba ujumbe gani, mzee huyo alimshangaza zaidi pale alipoanza kucheka kwa sauti ya chini chini huku meno kadhaa ya kinywa chake yakionekana. “Samahani nitakuchelewesha kidogo” hatimaye mzee huyo alisema, baada ya kuona Jacob ameshangazwa na kitendo chake cha kuachana na safari yao na kuanza kuelekea upande mwingine.

    Jacob aliangalia nyuma kuona kama lile gari alilohisi kuwa linawafuata kama lilikuwa bado linawafuta. Ndiyo! lilikuwa nyuma yao kwa tofauti ya magari mawili kati yao. Wakati Jacob anapapasa mfuko wake tayari kwa kutoa bastola yake, yule mzee naye aliongeza mwendo wa gari kwa ghafula!!

    Alizipita gari kama tatu hivi kwa kasi na kukata kulia kuingia barabara ya benki kuu akawa kama anaelekea Central Arusha. Hapo aliongeza mwendo zaidi kabla ya kupunguza kwa ghafula na kuingia kulia, akapita ofisi za TRA Arusha kwa mwendo wa kasi, hadi pale walipokuwa wakitazamana na jengo la AICC, hapo aliingia kulia akawa anateremka kuelekea round about inayounganisha barabara inayotokea ilipo Meat King, Benki kuu na Arusha City Council. Hakuingia kwenye round about, akakunja kushoto, alipita mbele ya ofisi za mkuu wa mkoa kwa mwendo wa kasi, akateremka kwa kasi hadi alipofika mnara wa saa hapo akakunja kushoto kuchukua barabara inayoelekea Impala hotel. Aliyafanya yote hayo huku lile tabasamu lake likiwa bado limeupamba uso wake. Mpaka wakati huo Jacob hakuwa amefanikiwa kuelewa maana ya tabasamu hilo la utata.

    Japo alionekana kuwa mtulivu zaidi kwenye kiti alichokuwa amekaa, lakini mambo kadhaa yalikuwa yakikitatiza kichwa cha Jacob Matata, tangu hapo alipokuwa ameshuka pale kiwanjani. Nadhani hata kama ungekuwa ni wewe, unaweza kuona kuwa mambo yanachanganya kweli. Kuja kwake Arusha aliifanya kuwa siri, sasa hawa waliokuwa wakilifuatilia gari hili alilopanda ni akina nani? Huyu dereva mzee kafanikiwa kuwakwepa, lakini hakuna aliyemwambia kuwa awakwepe na isitoshe amejuaje kuwa walikuwa wanawafuatilia wao? Hakuwa anajua Jacob ni nani. Kwa nini muda wote huu amekuwa akitabasamu pasipo kuongea neno lolote? Amweke kundi gani la wabaya au wema? Maswali yote hayo hakuyapatia majibu.

    Walifika Mlimani hoteli saa sita na nusu mchana. Wakati dereva huyo akitafuta mahali pa kuegesha gari, Jacob akatumia fursa hiyo kumwangalia na kuitalii sura yake. Alianza kuamini kuwa yawezekana akawa si dereva kama madereva wengine.

    Haikumchukua muda mrefu sana kuona tofauti, baada ya kuanza uchunguzi wake kwa mzee huyu, Jacob aligundua kuwa alikuwa amevaa sura ya bandia usoni.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Mara hii hamu ya kutaka kujua mzee huyu alikuwa ni mtu wa namna gani iliongezeka huku ikichanganyikana na wasiwasi wa kuwa huenda mzee huyu alikuwa ametumwa makusudi kuja kumpokea.

    Wakati anamaliza kuwaza hayo tayari mzee huyo alikuwa ameshaegesha gari na kusubiri abiria atoe ujira wake na kushuka. Baada ya kuwa ameshamlipa, Jacob alishuka kwa tahadhali kubwa maana mpaka hapo hakuwa anamwamini tena. Alianza kupiga hatua kuelekea ndani ya hoteli hii ya Mlimani.

    Kama ungefanikiwa kumwona usingepeta taabu kugundua kuwa alikuwa katika vita ya mawazo. Mawazo mengine yalikuwa yakimtuma amfuatilie huyu mzee huku mengine yakigoma. Baada ya mjadala mkali ndani ya kichwa chake aliona kuwa mzee yule anaweza kuwa ni mtego, hivyo ni vema apoteze nyayo zake toka kwa yeyote aliyekuwa akijua juu ya ujio wake.

    Alipofika mapokezi Mpelelezi Jacob Matata hakupata tatizo kupata chumba. Chumba alichopata kilikuwa orofa ya tatu namba 321. Ilimchukua dakika kadhaa mpaka pale alipouona mlango wa chumba alichokuwa amepewa. Kabla hajaingiza ufunguo kwenye kitasa cha mlango Jacob aliangalia ili kuona kama kuna mtu aliyekuwa anategemea au kusubiri kuona sura yake eneo hilo. Hakuona yeyote. Alingiza funguo katika kitasa na kuuzungusha, mlio uliotokea uliashiria kuwa mlango ulikuwa unasubiri mtu kuusukuma ili umruhusu aingie ndani. Jacob hakuusukuma wala hakuwa na haja ya kuingia ndani. Alichomoa ufunguo na kuanza kuondoka eneo hilo. Alipofika umbali fulani toka mlangoni hapo, alitafuta kona nzuri ya kuweza kujibanza.

    Huku akijifanya kama anayemsubiri mtu fulani, alikuwa anasubiri kuona kama kuna mtu angekuja kuchunguza kile chumba. Dakika kadhaa zilipita bila kuwa na dalili yoyote ya mtu kuchunguza chumba hicho. Jacob hakuona sababu ya kuendelea kusubiri, hivyo kwa kupitia njia za kughushi aliweza kutoka ndani ya Mlimani hoteli.

    Hapo nje alichukua taxi nyingine na kuomba apelekwe Paradiso hoteli. Hapo ndipo aliamua kuwa ndipo yangekuwa makazi yake kwa siku hiyo.



    * * *



    Baada ya kuoga na kupata kahawa katika mgahawa wa hoteli hii ya Paradiso, Jacob alijisikia vizuri hasa ukizingatia muda huo mji wa Arusha ulikuwa na baridi kali sana. Baada ya kupata kahawa hiyo alirudi chumbani kwake ili apange namna ya kuanza shughuli ya kuwasaka wanaopanga kufanya mambo ambayo kila mpenda amani angekuwa kinyume nao na inamaana alitakiwa kupambana na Max ‘the Fuse’.

    Alipoona kila kitu kiko sawa, alijilaza kiandani huku akifikiria ni wapi pa kuanzia. Kila alipofikiria hakuona kama angepata msaada wa haraka wa kumpa japo dondoo za mambo alivyo ndani ya Arusha. Polisi ndiyo wangeweza kumpa taarifa za haraka, lakini tayari alikuwa ameshapewa taarifa za kuuwawa askari kadhaa ikiwa ni pamoja na Inspekta Sogoyo aliyeuawa masaa machache yaliyokuwa yamepita. Sababu nyingine ya kutotaka kuonana nao ni ileile ya kutotaka kujulikana kuwa yuko Arusha. Japo alijua fika kuwa Polisi wangefurahi sana kusikia kuwa mtu kama yeye yuko Arusha kwa kipindi kama hiki ambacho mji huu unawaka moto.



    * * *



    Asubuhi hii Jacob aliamka mapema sana, alitoka kitandani na kuwasha televisheni iliyokuwapo chumbani hapo. Aliangalia taarifa za habari na matukio kupitia vituo mbalimbali vya televisheni.

    Jambo moja lililomfurahisha ni pale alipoona mwenyekiti wa mkutano ambao ulikuwa umepokea vitisho usifanyike, alisisitiza kuwa pamoja na yote yaliyokuwa yametokea Arusha lakini mkutano ni lazima uwepo. Pia alitoa wito kwa viongozi wote wa usalama wa nchi hizo kufanya jitihada zote kuhakikisha kuwa watu waliohusika na kutoa vitisho watafutwe na kukamatwa haraka iwezekanavyo.

    Jacob alitoka kitandani na kufanya mazoezi kidogo chumbani humo katika hali ya kuweka mwili kuwa ‘fit’ zaidi. Baada ya hapo aliingia bafuni kuoga. Muda mfupi baadae alikuwa ameshamaliza usafi na kuvaa, hivyo akawa tayari kwa kuondoka. Wakati akiwa amesimama tayari kwa kuondoka, simu yake ya mkononi iliita. Aliipokea.

    “Hallo nani na nikusaidie nini” Jacob aliuliza mara baada ya kubonyeza kitufe cha kupokelea.

    “ Unaongea na Mzee Edson Kinyaro hapa. Naomba tuonane, niko nje ya hoteli uliyofikia sehemu ya kuegeshea magari. Utanikuta ndani ya gari aina ya Landrover Discover ya bluu” Alipomaliza kusema kama kawaida yake alikata simu.

    Jacob akabaki na mshangao, alijiuliza ni namna gani mzee huyu alikuwa amejua kuwa alikuwa ameshakuja Arusha, kwani katika maongezi kwa njia ya simu wakati Jacob alipokuwa Dar hakukumbuka kuwa alimwambia kuwa angekuja Arusha. Sasa alijuaje kuwa Jacob tayari ameshafika na tena ni kwenye hoteli ya Paradiso baada ya kuikwepa ile ya Mlimani.

    Ni kweli alikuwa anamfahamu sana mzee Edson, lakini taratibu za kazi hazimruhusu kuonana na watu wakubwa kama Edson katika uwanja wa mapambano. Edson ni hazina ya taifa kwani licha ya kuwa ameshastaafu lakini alikuwa na taarifa ambazo ni siri ya kiwango cha juu kwa taifa. Hivyo kwa mpelelezi kama yeye haikuwa vema kuhatarisha maisha ya mzee huyo kwa wakati ambao ameshahisi kuna kila dalili ya hatari katika mji wa Arusha. Pia alifikiria kuwa kwa vile yeye na Edson wanamjua Max, mara moja Max hatochelewa kuyaondoa maisha ya Edson kama akihisi kuwa ameshajua kuwa anahusika na balaa linaloendelea Arusha.

    Baada ya kufikiri kwa kina Jacob Matata akaonelea ampigie simu ili amwambie kuwa hakuwa tayari kuonana na yeye na wala asingependa mzee huyo aendelee na tabia ya kumfuatafuata. Alichukua tena simu yake, ili kwa kutumia namba alizokuwa amepigiwa aweze kumpigia mzee huyo na ‘kumchimba mkwara mzito’. Alianza kuangalia orodha ya simu alizokuwa amepokea siku hiyo. Alisonya kwa nguvu pale alipofikia ilipokuwa namba ya simu aliyokuwa amepigiwa na mzee Edson na kukutana na neno ‘number withheld’ ikimaanisha kuwa mpigaji alikuwa ameficha namba yake isijulikane na mpokeaji.

    .

    Baada ya kujiuliza kwa upya akaazimia kuitikia wito wa mzee Edson na wakionana ndipo amweleze kuwa si salama kwake kujiingiza kwenye kisa hicho. Hata kama angekuwa na hatari, hatari ndio ilikuwa kazi yake na kitendo cha kukubali kuja Arusha ilimaanisha kuwa alikuwa tayari kukutana na hatari kama hizi. Hivyo ingekuwa ni ujinga kuogopa hatari wakati alikuwa amekuja kwenye hatari. Kwa hadhali kubwa aliadhimia kwenda kumsikiliza mzee Edson. Alichukua bastola yake ‘Automatic’ iliyotengenezwa Urusi na kuificha kati ya moja ya mifuko yake ya siri.

    Wakati Jacob akiwa anataka kutoka chumbani humo ili kwenda kuonana na Mzee Edson, mara mlango wa chumba chake uligongwa!http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kabla hata hajafikiria nini cha kujibu au kufanya, mlango ulifunguliwa na mtu akaingia. Alipoingia tu tayari bastola ya Jacob Matata ilikuwa usawa wa paji la uso wa jamaa huyo.

    “Karibu ndani na uketi huku mikono yako ikiwa imewekwa juu, ukishindwa kufanya hivyo ni imani yangu kuwa hutanilaumu kwa lile nitakaloamua kukufanya” Jacob alisema huku akitumia mguu wake kuusukuma mlango wa chumba hicho ambao ulitii na kujifunga.

    Sura ya mtu huyu haikuwa ngeni sana kwa Jacob japo ilikuwa na mabadiliko madogo. Lakini aliweza kutambua kuwa alikuwa ni yule mzee aliyembeba kwenye gari lake jana toka uwanja wa ndege alipowasili Arusha.

    Jambo moja bado lilikuwa linamtatiza Jacob kuhusu huyu mzee, kama ilivyokuwa jana alipokuwa ndani ya gari yake. Mzee huyu tabasamu fulani lilikuwa liko usoni kwake. Pamoja na kuwa bastola ya Jacob ilikuwa usawa wa uso wake lakini hakuonyesha hata chepe ya wasiwasi. Alitembea mpaka kwenye kochi lililokuwa chumbani humo na kukaa juu yake. Aliweka chini mkoba aliokuwa amekuja nao.

    “Bwana Jacob najua kuwa umepata wito huko nje kwa hivyo sitakuwa na muda wa kupoteza zaidi. Ila nimeshataarifiwa kuwa kazi na safari hii ya kuja Arusha haikuwa katika mpangilio wako. Lakini kwa vile wewe ni mzalendo na mtanzania wa vitendo ndio maana umekubali kukatiza likizo yako na kuja kufanya kazi hii ya kusambaratisha kikundi hiki kinachotishia watu wasifanye yaliyo mema kwa Afrika” Aliongea mzee huyu katika sauti ya utulivu huku macho yake yakiwa sambamba na yale ya Jacob. Macho yake yalionyesha kitu fulani. Kitu hicho kilitambulika kwa Jacob kuwa mzee huyu alikuwa ni ‘mzee wa kazi’ aliyeiva sawasawa.

    “Nimekuja hapa kwa ajili ya mambo matatu” aliendelea “moja; naamini kabla hujaondoka Dar Bi. Anita alikutaarifu juu ya mtu aliyemteua kukupa msaada pale utakapohitaji. Basi mtu huyo ndiye mimi.

    Jambo la pili ni kukuhadhali kuwa watu hawa tayari wana taarifa juu ya uteuzi huu na wameshajua kuwa umeshaingia Arusha. Kama unakumbuka jana wakati nimekuja kukupokea walijaribu kutufuatilia bila mafanikio. Hii inaonyesha kuwa kuna mtu tayari ameshavujisha habari juu yako.

    Tatu; Bi. Anita ameniagiza kukuletea vifaa ambavyo anaamini kuwa vinaweza kukusaidia katika kuendesha shughuli hii. Na ningekushauri kwa sasa kabla ya kutoka humu chumbani ujaribu kujibadilisha sura kwani unatafutwa sana na hawa watu” Alipomaliza kusema hayo Mzee huyo alimkabidhi Jacob mkoba mmoja mdogo uliokuwa umesheeni vitu mbalimbali vya kipelelezi. Jacob alivipokea huku akiwa bado ameshikilia bastola yake, hakuwa tayari kumwamini yeyote kwenye mazingira na wakati kama huo.

    “Najua una hamu ya kujua mimi ni nani, lakini naona huu si muda muafaka wa kuongelea hilo. Ila utakapokuwa unanihitaji namba zangu za simu ni hizi hapa na mara kwa mara nitakuwa naegesha gari langu aina ya caldina ya rangi nyekundu pale Phillips jirani na zilipo ofisi za Pan African Movement. Mara zote nitakuwa hapo kwa ajili yako, mpaka hapo kazi hii itakapokuwa imekamilika. Pia nimeandaa nyumba ambayo unaweza kuifanya kama kambi yako ya mapumziko, hivyo unaweza kuniona na nikakuonyesha nyumba hiyo. Nakutakia mafanikio katika kazi ya hatari na ngumu iliyoko mbele yako, ila uwe makini ukijua fika kuwa adui yako anajua uwezo wako na anajua kuwa tayari uko Arusha. Wasingependa uendelee kuwa hai, ili yale waliyoazimia kufanya yatimie”. Alisema maneno hayo huku akisimama tayari kwa kuondoka. Jacob alijikuta anakosa hata neno moja la kuuliza, badala yake akawa anamwangalia mzee huyu kama mtu aliye katika maono ya kushangaza kama yale ya Musa na kijiti kilichokuwa kikiwaka pasipo kuteketea.

    Yule mgeni wa ajabu alipotoka nje ndipo Jacob akaanza kuangalia ndani ya mkoba aliokuwa ameachiwa ili kuona kulikuwa na nini ambacho angehitaji kukitumia kwa wakati huo. Aliviangalia vyote kwa makini. Kwa kutumia mbinu fulani na vifaa alivyokuwa ameletewa, baada ya muda mfupi tayari alikuwa ameshabadilisha sura yake kwa moja kati sura za bandia alizokuwa amezikuta katika mkoba huo.

    Baada ya kuhakikisha kuwa alikuwa tayari kwa lolote ndipo akaona kuwa ulikuwa ni wakati muafaka wa kwenda kumwona mzee Edson ambaye bila shaka alikuwa bado akimsubiri nje ya hoteli hiyo. Hakujua kuwa ni kwa vipi watu hawa walikuwa wanajua juu ya nyendo zake kwa urahisi kiasi hicho.

    Alifungua mlango wa chumba ili atoke, kisha akaufunga nyuma yake kabla ya kuanza kushuka ngazi kuelekea chini. Akili yake ilikuwa ikimnong’oneza kuwa kazi ndiyo ilikuwa inaanza.

    Alipita eneo la mapokezi na kutokezea sehemu iliyokuwa na mgahawa. Hapo ndipo akakumbuka kuwa alikuwa hajapata kifungua kinywa. Akaona ni bora akamwone mzee Edson na kumwambia kuwa amsubiri ili apate kifungua kinywa au kama na yeye alikuwa hajapata basi wapate kwa pamoja.

    Jacob Matata tayari alikuwa ameshafika nje ya hoteli na kuanza kuelekea ilipokuwa sehemu ya kuegeshea magari ya wateja au wahusika wa hoteli. Aliangaza macho yake sehemu hiyo, akaiona gari aliyokuwa ameelekezwa na mzee Edson.

    Wakati anapiga hatua kuelekea mahali ilipokuwa gari hiyo, Jacob hakuamini macho yake pale alipoona gari ya mzee Edson ikisambazwa vipande vipande. Ndiyo!! alikuwa ameona vizuri. Lile gari alilokuwemo mzee Edson lilikuwa limeshambuliwa na bomu. Wakati Jacob akiwa bado anafikiri nini cha kufanya mara akasikia mlio wa gari ikiondoka kwa kasi katika eneo hilo la hoteli na kuacha gari ya mzee Edson ikiwa inateketea vibaya. Alihisi kuwa gari hiyo iliyoondoka kwa kasi, ambayo hata hivyo hakufanikiwa kuiona ndiyo iliyokuwa ikitumiwa na waliofanya shambulio hilo.





    * * *

    Dakika chache baadae, gari ya zima moto na askari wake walifika eneo hilo na kuanza kuzima moto uliokuwa kiteketeza gari ya mzee Edson kwa kasi, huku mzee Edson akiwa ndani yake.

    Jacob alijikuta akianza kujilaumu kwa kitendo chake cha kujiuliza uliza kuonana na mzee Edson, kwani labda asingemchelewesha asingepatwa na hayo yote. Lakini tena akajirudi kuwa wenda angewahi kuingia ndani ya gari hiyo angekuwa anateketea pamoja na mzee Edson kwani washambuliaji wasingesita kumuangamiza yeyote ili mradi tu wafanikishe azma yao ya kuutoa uhai wa mzee Edson. Inaonekana kuna jambo ambalo mzee Edson alikuwa anajua au aliingilia kuhusu jamaa hawa ndiyo maana wakaamua kuutoa uhai wake.

    Askari wa zima moto walikuwa wamefanya kazi yao kwa ujasiri na ustadi mkubwa, kwani baada ya muda mfupi tu walikuwa wameshafanikiwa kuuzima moto uliokuwa ukiteketeza gari ya mzee Edson na maisha yake mwenyewe. Baada ya kumaliza kuuzima moto waliingia ndani ili kuona kama kulikuwa na mtu ndani yake.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    * * *



    “Buriani Edson, buriani Bosi” Max alisema baada ya vijana wake kumtaarifu kuwa wameshamuua Edson Kinyaro.

    Ni kwamba; Kwa vile walikuwa wanafuatilia na kusikiliza kila simu iliyopigwa na kupokelewa na Mzee Edson, kundi hili lilifanikiwa kunasa mazungumzo ya Edson na Jacob Matata siku ile Jacob alipokuwa ametoka ofisini kwa Bi. Anita kukabidhiwa kazi ya Arusha.

    “Nilijua tu, Edson kwa vile ananifahamu vema lazima angekimbilia kuomba msaada toka kwa Jacob Matata” Max alisema baada ya Edson kuwa amekata simu kukwepa maswali zaidi toka kwa Jacob.

    “Umesikia jinsi Jacob alivyoshituka sana kusikia The Fuse uko Arusha??!!! Mmoja wa watu hao alisema huku akimwangalia Max.

    “Ananijua, anajua haniwezi ndiyo maana unaona hataki hata wazo la Edson kuwa aje Arusha. Japo sijaonana na Jacob muda mrefu lakini najua haniwezi katu. Sijui hata alibahatishaje kumuua Kiroboto, nadhani natakiwa nisome kile kitabu cha HEKA HEKA (kitabu hiki pia kimeandikwa na Japhet Nyang’oro, kitafute) ili nione Jacob alifanikiwaje kumuua pacha wangu Kiroboto na staili yake ya Amazon Cat.” Max alijigamba huku wengine wakimsikiliza. Hakuna aliyebisha maana wote waliokuwa hapo wameshawahi kufanya kazi kama hii na Max katika vipindi tofauti tofauti nchi mbali mbali katika bara hili la Afrika. Walijua kuwa Max alikuwa moto wa kuotea mbali.



    Baada ya kuwa wamesikiliza mazungumzo ya Jacob na Edson ndipo sasa walianza kufuatilia mawasiliano kwenye simu za wawili hao. Waliweza kujua siku ya kufika Jacob Matata, wakamfuata uwanja wa ndege ili wajue angelala hoteli gani halafu usiku wamfungie kazi. Lakini walishangazwa na tabia ya dereva Taxi aliyewachenga na kuwafanya wasimpate Jacob Matata. Hata hivyo walipata taarifa kuwa alikuwa amefikia Mlimani Hotel, ambaho hata hivyo walipoenda usiku waliambulia patupu. Hivyo simu ambayo Edson Kinyaro alimpigia Jacob iliwapa ramani mpya, bila kuchelewa wakawa wamefika Paradise Hotel na kufanikiwa kuliona gari la Edson Kinyaro kama alivyokuwa amemuelekeza Jacob Matata kwa njia ya simu. Walisubiri kwa muda.

    “Ningependa muwamalize wote papo hapo, ila namjua Jacob Matata ni kama huwa ana hirizi hayawani yule” Max alisema alipotaarifiwa kuwa Edson tayari yuko kwenye kumi na nane zao - on target na kuwa wanaweza kufanya lolote.

    “Subirini tena kama dakika kumi, Jacob asipotokezea, mmalizeni huyo mzee halafu tutajua namna ya kumalizana na Jacob. Hans wewe waache wenzio kwenye gari, nenda hotelini ukasaidie wanaofuatilia nyendo za Jacob, akiwemo malaika wa giza” Max alitoa maelekezo ya ziada.

    Dakika kumi na moja baadaye ndipo akapewa taarifa kuwa wameshamwondoa Edson, ila hawakuwa wamefanikiwa kummaliza Jacob Matata, hakuonekana.

    “Nilijua, si rahisi kumtega Jacob kama mtu ategaye kuku. Yule ni fundi na hutegwa na mafundi zaidi yake, ila najua udhaifu wake. Anapenda nyonyo sana yule. Mbwa mwenye mnofu mdomoni hapigi kelele” Max alijisemea huku akitupia kinywani vipande kadhaa vya Kahawa na kuendelea kujitafuna. Hii ni moja ya tabia zake, hupenda kutafuna Kahawa ambazo hazijasagwa ila zilizokaangwa. Hii humfanya muda wote anukie harufu ya Kawaha.



    * * *

    Maiti ya mzee Edson Kinyaro ilitolewa kwenye gari iliyokuwa imetekea na kuingizwa ndani ya gari ya kubebea wagonjwa. Kuona hivyo Jacob naye akaingia kwenye gari yake ambayo alikuwa amefanya utaratibu wa kuikodisha tangu akiwa Dar. Alikuwa amewasiliana na kampuni ya kukodisha magari ya hapo mjini Arusha ijulikanayo kama Bamboo Car Rental na kukodisha hilo gari. Hivyo asubuhi hiyo akawa amewaamewaomba waiegeshe mbele ya Paradise Hoteli kisha wapeleke ufunguo sehemu ya mapokezi. Meneja wa Bamboo Car Rental alikuwa anajuana na Jacob Matata. Alikuwa ameamua kuufuatilia mwili wa marehemu mzee Edson ili yumkini aweze kuwafahamu hata ndugu zake tu ambao aliamini kuwa wangefika hospitali.

    Baada ya Kama dakika nne hivi baadae tayari Jacob alikuwa ni miongoni mwa watu walikuwa katika hospitali ya Mount Meru. Mwili wa mzee Edson tayari ulikuwa umeshapelekwa kwenye chumba maalum cha kuhifadhia maiti cha hospitali hiyo.

    Jacob alikuwa amesimama eneo ambalo angeweza kumwona kila aliyekuja kuuona mwili wa marehemu, mzee Edson.

    Wakati akiwa hapo akawa anafikiria juu ya kitendo hiki kilichokuwa kimetokea dakika chache sana mbele ya macho yake huku waliofanya wakimwacha kama mtu aliyekuwa amepigwa sindano ya ganzi. “Kweli wamedhamilia lakini ama zangu au zao. Huyu atakuwa Max, maana ndiyo zake mshenzi yule, hutoa roho za wenzake kama kama vile mtu auaye mbu aliyenasa kwenye chandarua.” Jacob alijikuta akijisemea kwa sauti ya kuweweseka. Alijua fika kuwa ili kutimiza azma yake ilihitajika apite katika njia za hatari na apambane kiume. Na mwisho wa siku apambane na Max The Fuse. Hakuhitaji papara wa kubahatisha katika oparesheni hii, maana haraka ingeweza kumpeleka pabaya. Alipomfikiria Max, zile hisia za Ben, “The Kiroboto” kwenye HEKA HEKA zikawa zinamjia, mwili ukamsisimka, akajisikia raha, maana hatari ndiyo ilikuwa ajira yake.

    Taratibu na kwa mbali akili yake ikaanza kumletea sauti na maneno aliyoambiwa na mzee Edson wakati bado akiwa Dar. Ulikuwa ni kama wosia ambao mzazi alikuwa amemwachia mwanae. “Kosa la kiufundi hugunduliwa na fundi lakini pia hurekebishwa na fundi”. Ndivyo alivyokuwa amesema mzee Edson.

    Alijiona kama mtu aliyewiwa kitu na mzee huyo. “Lazima nitimize yale aliyokuwa akiyafikiri kuwa ilikuwa ni lazima yafanyike”Alijisemea kwa mara nyingine.

    Wakati Jacob akiwa katika hali hiyo ya kufikiri na wakati huo huo akisubiri jamaa wa mzee Edson, mara gari aina ya Hiace ndogo iliingia eneo la mbele la hospili hiyo, kwa Arusha hujulikana sana kama ‘kifodi’. Baada ya gari hiyo kugesha aliteremka mama mmoja aliyekuwa akilia sana. Wanawake wengine wawili walikuwa wameshikilia. Mara Jacob alimtambua kuwa ndiye mke wa mzee Edson. Alimkumbuka, kwani kama alivyosema mzee Edson wakati anaongea na Jacob kwa simu akiwa Dar; Jacob alishauriwa na Mzee Edson na kupelekwa shule za fani ambayo Jacob anaifanyia kazi leo hii. Wakati huo Edson alikuwa mkuu wa usalama wa Taifa.

    Mama huyo aliingia ndani. Jacob aliendelea kubana hapo alipokuwa awali, ili aweze kujua nini kingeendelea. Kama dakika tatu baada ya kufika kwa mke wa mzee Edson, gari aina ya Nissan Teranno iliegesha jirani kabisa na ilipokuwa gari iliyokuwa imemleta mke wa mzee Edson. Ilipoegesha hakushuka mtu, hisia za hatari zikaujaa mwili wa Jacob, lakini kwa jinsi alivyokuwa amebana aliamini kuwa ingechukua muda kwa mtu kumuona na kuamini kuwa alikuwa anafuatilia jambo hili.

    Mara Alitelemka Msichana mmoja mrembo sana toka ndani ya hiyo gari. Dada huyu alikuwa na sifa ambazo zingemfanya mwanamume yeyote amwite mrembo. Aliposhuka tu aliangaza macho yake hapa na pale. Mara macho yake yakagongana na yale ya Jacob. Akatabasamu. Lakini inaonyesha hakutaka ijulikane na Jacob kuwa amemuona. Alianza kutembea kuelekea ndani, lakini tofauti na wengine yeye alitumia njia hii ambayo Jacob alikuwa amebana. Nakwambia ungemwona wakati akitembea ndipo ungejua ni kwa nini Jacob alikuwa amesisimkwa pande zote mara baada ya kumwona dada huyu. “Nimeshawahi kuona wasichana mbalimbali katika nchi mbalimbali nilizowahi kufanya kazi lakini nadhani huyu ni kiboko yao”. Jacob alijiwazia.

    Alikuwa ameshakaribia kabisa na alipokuwa amesimama Jacob Matata. Kuona hivyo, Jacob akajiweka tayari kwa lolote maana muda kama huu kulikuwa na kila dalili za mauti hasa ukizingatia kuwa siku hizi waharifu wa kimataifa ni wanawake tena warembo kama huyu anayemwona. Jacob alijiona kama mtu aliyeko katika mdomo wa mauti, ambapo ukizubaa tu unamezwa na hutoonekana tena.

    Mrembo huyo tayari akawa ameshafika pale alipokuwa amesimama Jacob. Hapo alifanya jambo moja, alimgeukia Jacob na kumpa kitu kama bahasha. Lo! Ungemwona Jacob Matata jinsi mapigo ya moyo yalivyokuwa yakimuenda kasi ungemuhurumia. Si kwamba alimwogopa msichana huyo, la, ila macho yake na tabasamu alilotoa wakati akimkabidhi bahasha hiyo vilimfanya ahisi pumzi zikimtoka.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



     Ghafula Jacob akajikuta anavutiwa na msichana huyu japo hakuwa anajua ni nani na ilimjuaje. Kumbuka wakati huo wote Jacob bado alikuwa katika sura ya bandia aliyokuwa amevaa kabla hajatoka hotelini.

    Baada kukabidhi bahasha kwa Jacob, msichana huyo hakuendelea sana kwenda upande aliokuwa akielekea. Alirudi mpaka ilipokuwa gari yake. Hapo alisimama huku akimwangalia Jacob. Hii iliashiria kuwa alihitaji Jacob aisome ile barua wakati huohuo na kuitolea maamuzi.

    Jacob aliifungua hiyo bahasha na kuanza kuisoma kwa jicho moja huku moja lililobaki likiwa linamwangali mrembo huyo. Maana aliona isije ikawa ni mtego kwa hivyo wakati anasoma ndiyo ikawa nafasi nzuri kwa yule msichana kufanya vitu vyake dhidi yake. Hivyo jicho moja lilisoma na jingine lilikuwa likimchunga. Kwa mtu kama wewe msomaji zoezi hilo lingekuwa gumu na nina hakika usingeliweza, lakini kwa mtu kama Jacob ilikuwa ni zoezi dogo kabisa.

    Ndani ya bahasha kulikuwa na karatasi yenye ujumbe ufutao; ‘Jacob naomba tuwe na mazungumzo nawe japo kidogo katika sehemu utakayoichagua wewe. Niko hapa nasubiri jibu’. Alipomaliza kusoma tu Jacob alimkumbuka mzee Edson ambaye muda mfupi kabla ya kifo chake alikuwa amempa ujumbe kama huo kwa njia ya simu.

    Alimwangalia yule msichana ambaye alikuwa bado akimwangalia. Kuona anaangaliwa na Jacob dada huyo alitabasamu tabasamu ambalo Jacob hakupata shida kugundua kuwa kuna kitu lilikuwa linakosa. Aliikunja hiyo karatasi na kuiweka mfukoni. Tayari alikuwa amepata uamuzi.

    Kwa tahadhakli kubwa alipiga hatua mpaka pale alipokuwa amesimama yule dada. Kisha akaonyesha ishara ya kuwa amekubali kuondoka. Kuona hivyo msichana huyo akataka kufungua mlango ili Jacob aingie.

    Wakati anafungua mlango tayari bastola ya Jacob Matata ilikuwa imeshagusa kisogo chake. “Mikono juu na usilete ujanja wowote, kama una silaha yoyote ni wakati wa kuikabidhi kabla sijakagua na kukukuta nayo” Jacob alisema huku akinyoosha mkono mmoja kama ishara ya kuwa tayari kupokea silaha yoyote ambayo alikuwa nayo. Bila kusita msichana huyo alitoa bastola moja na kuikabidhi kwa Jacob. Pamoja na kutoa Bastola hiyo, lakini msichana huyo hakuonyesha wasiwasi wowote.

    Kwa namna ya ajabu, Jacob alimchukua judo moja kali msichana huyo, alipokujatahamaki alijikuta yuko ndani ya buti ya gari lake. Jacob aliifunga haraka buti hiyo na kuingia upande wa dereva. Aliindoa gari hiyo kwa kasi toka hapo hospitalini.

    * * *



    Safari ya Jacob Matata na mateka wake iliishia kwenye msitu mdogo nje kidogo ya mji wa Arusha, eneo la Makumira jirani na shule ya sekondari makumira. Jacob alikuwa ameamua akubaliane na ombi la msichana huyo la kutaka maongezi naye kwa njia hii. Aliegesha gari sehemu fulani na kushuka huku bastola yake ikiwa mkononi. Aliiendea buti na kufungua.

    Jacob alipigwa na mshangao pale alipokuta yule msichana hayupo. Ametoka vipi na saa ngapi? Wakati bado akiwa katika hali ya kushangaa, mara akasikia mlio wa gari likija upande aliokuwepo. Kwanza alidhani ni mkulima alikuwa anakuja kuangalia mashamba yake. Eneo hilo lilikuwa na mashamba makubwa yaliyokuwa yanamilikiwa na watu wenye uwezo kifedha.

    Lakini wazo hilo lilitoweka pale nilipoiona gari iliyokuwa ikija. Ilikuwa ni ile gari ya kukodi ya Jacob aliyokuwa ameiacha hospitali kabla ya kutumia hii ya yule dada. Mara moja Jacob akajua kuna hatari. Gari hiyo haikusogea sana sehemu aliyokuwa amesimama. Iliegesha mbali kidogo.

    Jacob aliweza kumwona msichana aliyekuwa akishuka toka ndani ya gari hiyo. Hakuwa mwingine ila yule mrembo aliyekuwa akidhani yuko ndani ya buti ya gari aliyokuwa ameendesha yeye Jacob. Baada ya kushuka alianza kutembea kuelekea pale alipokuwa Jacob, kama kawaida yake dada huyu hakuonyesha wasiwasi wowote.

    Tayari alikuwa ameshafika alipokuwa amesimama Jacob.

    “Samahani kwa kuvunja utaratibu wako, lakini sikuona kuwa ni njia nzuri ya kumchukua mtu mwema kama mimi. Usijali hata hivyo nimejileta mwenyewe tayari kwa mazungumzo na wewe japo wewe hakupenda nije kwa njia hii” Alisema mrembo huyu ambaye sasa hakusita kuonyesha sura yake ya huzuni. Jacob aliposoma sura yake kwa makini hakuchelewa kugundua kuwa msichana huyo alikuwa na maswahibu mengi yaliyokuwa yakimsibu. Alikuja akasimama pale alipokuwa amesimama Jacob na kunyamaza kimya kana kwamba kuna maagizo aliyokuwa akiyasubiri.

    Jacob alishangaa kuona kuwa mrembo huyu alionyesha kuwa alikuwa anamfahamu sana japo mwenyewe hakuwa akimfahamu.

    Ni wakati Jacob anataka kuanza kuongea ndipo alipoisikia sauti tamu ya msichana huyo ikipenya masikioni mwake na kusema.”Jacob Matata kijana unayeogopwa sana na kila aliyeadui wa haki. Mtu mwenye sifa zote za kuitwa komandoo na mzalendo wa hali ya juu kabisa. Mtu ambaye Tanzania na Afrika kwa ujumla inajisifia kuwa naye. Mwaka 2004 ulikuwa kwenye timu ya wapelelezi waliokuwa wameteuliwa na Afrika kuunda timu ya wapelelezi wa balaza la usalama la umoja wa mataifa kwenda kuchunguza uwezo wa kisilaha wa nchi ya korea ya kaskazini.

    Wakati ulipokuwa Ubelgiji ndipo kwa mara ya kwanza ulipokuatana na jaji Mark Gordón. Kama utakumbuka jaji alikuwa ameoa mwanamke wa kitanzania na walikuwa na mtoto mmoja tu wa kike. Jaji Mark Gordón aliuawa hapahapa Arusha siku mbili zilizopita. Sababu kuu ya kuuawa kwa Jaji Mark Gordón ilikuwa ni juu ya msimamo wake katika masuala kadhaa yanayozikabili nchi za eneo hili kwa wakati huu …” Wakati akiendelea kuongea Jacob aigeuka na kumwangalia vizuri msichana huyo na ndipo akaikumbuka sura yake.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hivyo akamdakia na kusema. “Merina Mark Gordón msichana pekee wa jaji Mark Gordon. Msichana uliyehitimu mafunzo ya juu kabisa katika fani ya upiganaji. Ni msichana aliye na shabaha ya kushangaza na kipawa cha ajabu katika mtindo wa karate”. Alipofika hapo Akasita na kumgeukia tena, safari hii akaenda kusimamia mbele yake. “Pole sana kwa yote yaliyokupata juu ya kifo cha baba yako” Jacob aliposema hivi kwa vile Merina alikuwa karibu naye sana alijiegemeza kifuani kwake huku machozi yakimtoka. Kumwona msichana mrembo kama huyu akilia kwa sababu ya ukatili wa watu wasiopenda utu wala Amani, Jacob alijikuta chuki yake juu ya watu kama hawa ikiongezeka mara dufu.

    “Ulijuaje kuwa ni miye maana hii sura niliyonayo leo ni ya bandia? Hatimaye Jacob alihoji

    “Nilikufuatilia tangu ulipokuwa unatoka chumbani hotelini kwako” Merina alijibu huku akiwa bado kajiegemeza kifuani kwa Jacob. Jacob alitumia fursa hiyo kuangalia uso wa msichana huyo kwa karibu zaidi. Jacob alishangaa jinsi msichana huyu alivyokuwa kajaaliwa. Jacob alipofikiri aligundua kuwa yawezekana ni kwa sababu ya mchanganyiko wa Wazazi wake. Ambapo kama ulivyosikia baba yake ni mzungu ambaye ndiye jaji Mark Gordón, na mama yake ni mbulu wa mkoa wa Manyara. Jacob aliweza kuhisi joto la Merina kupitia kifuani kwake ambapo Merina alikuwa amejiegemeza wakati huu.





    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog