Search This Blog

Thursday 27 October 2022

MUUAJI ASAKWE - 4

 









    Simulizi : Muuaji Asakwe

    Sehemu Ya Nne (4)





    MTAA mzima wa Shariff Shamba, Ilala, ulikuwa kimya kabisa usiku ule wa aina yake. Akiwa ni askari shupavu anayelala kiaskari, ilipotimu majira ya saa saba za usiku, Kachero Inspekta Malik Mkoba alishtuka kutoka usingizini, ikiwa ni baada ya kuusikia muungurumo wa gari lililokuwa linapita katika ule mtaa mdogo usiokuwa na jina, jirani kabisa na ukuta wa uzio wa nyumba yake.



    Ukweli ni kwamba haikuwa kawaida kwa gari kupita katika mtaa huo usiku mwingi namna hiyo, hivyo machale yakamcheza Malik na kuanza kuhisi hali ya hatari. Akanyanyuka kutoka hapo kitandani, halafu akaliendea dirisha kubwa lililokuwa upande unaotazama barabarani karibu na uzio wa ukuta ulioizunguka nyumba yake. Akalifungua pazia na kuchungulia nje, ambapo aliweza kupaona viziri kwa kupitia kwenye matundi yaliyokuwa kwenye uzio.



    Baada ya kuchungulia, akaliona gari moja dogo aina ya Toyota Corolla lenye rangi nyeupe, limesimamishwa mbali kidogo na ilipo nyumba yake, chini ya mti wa mkungu. Pia,  sehemu iliyokuwa na miti ya muarobaini iliyofungamana na kufanya kuwe na giza kiasi. Hakuyabandua macho yake katika gari hilo, na baada ya muda akawaona watu wawili wakishuka, wote  wakiwa wamevalia mavazi yaliyoshabahiana na giza, pamoja na kofia kubwa zilizoweza kuficha sura zao.



     Kwa usiku ule watu hao walikuwa wanatisha sana, na waliposhuka, wakaanza kutembea kwa mwendo wa taratibu kuifuata nyumba yake. Wotewalionekana kuwa na silaha, Robi alikuwa na bastola mkononi na Chogolo alikuwa amekamata bunduki fupi aina ya ‘Uzi Gun,’ iliyotengenezwa nchini Israel. Kwa tahadhari kubwa, Malik akajitoa pale dirishani na kuiendea bastola yake iliyokuwa imesheheni risasi, halafu akarudi hapo dirishani na kujiweka tayari kwa lolote litakalotokea! 



    Watu hao waliokuwa wanaijongelea nyumba yake walikuwa ni Robi na Chogolo, vijana wa John Bosho, ambapo alikuwa amewatuma kumsaka yeye tena, na kuhakikisha wanammaliza baada ya kumkosakosa mara ya kwanza! Walitembea hadi walipofika karibu na ukuta wa uzio, ambapo palikuwa na mti mmoja mwingine wa mwembe. Ni mti ambao matawi yake yalikuwa yameingia hadi sehemu ya ndani ya ua ule. Hivyo wakaupanda mti huo kwa ufundi mkubwa na kutua ndani bila kishindo, na baada ya kutua ndipo walipouendea mlango wa kingilia mle ndani.



    Ukweli ni kwamba mambo yao walikuwa wakiyafanya kwa utulivu wa hali ya juu kiasi kwamba hata majirani wa nje hawakuweza kujua zaidi ya yeye Malik. Mara Malik akasikia mlango huo wa mbele kabisa, unaotokeza sebuleni ukifunguliwa kwa kutumia ufunguo bandia, tena kwa utaratibu bila kufanya kelele za aina yoyote. Baada ya mlango kufunguliwa, akaona watu wale wakiingia hadi pale sebuleni na kusimama huku wakiongea kwa sauti ya chini, kuashiria kwamba walikuwa wanakitafuta chumba cha anacholala.



    Pale alipokuwa amesimama kachero Inspekta Malik, alikuwa akiwaangalia tu, na jirani yake palikuwa na swichi maalum, ambayo ikiwashwa hutoa mlio wa king’ora, kwa ajili ya kudhibiti wezi, au jambo lolote la hatari linapotokea! King’ora hicho alikuwa amekifunga muda mrefu sana kwa ajili ya kujihami, akiwa kama askari aliyeamua kuishi uraiani. Na kweli siku hiyo ndipo alipoona alifanya la maana baada ya kuingiliwa na wale wakora wawili, Robin na Chogolo. Hivyo, kabla Robin a Chogolo hawajanyanyua hatua, Malik akabonyeza kile king’ora ambacho kilianza kutoa mlio mkali sana, kitu ambacho kiliwafanya washtuke katika giza lile!



    Chogolo na Robi wakaangaliana mara baada ya kuusikia mlio huo wa king’ora, ingawa hawakuonana hapo sebuleni kutokana na giza! Wakaona usalama wao ukiwa mdogo mara baada ya kuingia ndani ya himaya hiyo ya mpiganaji mahiri!



    “Robi!” Chogolo akaita kwa sauti ndogo!



    “Sema mtu wangu!” Chogolo akasema huku akiyatumbua macho yake katika giza!



    “Unaona hatari inayotukabili lakini?”



    “Ni kweli naiona mshikaji, ni sawa na kuingia katika choo cha kike!”



    “Jamaa kajiandaa, na siyo muda mrefu atatunyeshea mvua ya risasi!”



    “Ni kweli! Tuanze!”



    Baada ya Robin a Chogolo baada kushauriana, waliamua kutoka mle ndani kwa kasi, huku kile king’ora kikiendelea kulia. Wakaufikia uzio wa ukuta ambao waliuruka na kutua nje kisarakasi, na kulikimbilia gari lao ambalo lilikuwa umbali mfupi tu kutoka kwenye nyumba hiyo. Walipolifikia wakapanda haraka haraka na Robi akaliondoa kwa mwendo wa kasi kwa kuufuata mtaa ule mdogo na kupotea gizani!



    Hapo ndipo Kachero Malik alipojitoa mafichoni na kwenda kuufunga ule mlango mkubwa kama ulivyokuwa mwanzo ikiwa ni baada ya kukizima kile king’ora alichofunga. Hali ikarudi shwari kama mwanzo kama vile hakikutokea chochote, hivyo akaamua kufanya uchunguzi wa awali, na akaona kuwa hakuna kitu chochote kilichoguswa pale sebuleni, zaidi ya mlango ule mkubwa, uliofunguliwa kwa ufunguo bandia.



    Pia, Kachero Inspekta Malik aligundua kuwa watu wale walipitia kwa kuuruka uzio wa nyumba yake kitu ambacho kiliwafanya wafanikiwe kuufungua mlango ule. Kutokana na hali hiyo, akajua kuwa vita vilikuwa vimeanza, ambapo aliunganisha tukio hilo la hapo nyumbani kwake, na lile la kuvamiwa ndani ya baa ya Kimicho, usiku usiku wa siku ile. Pia, aliunganisha na tukio la mauaji ya mwanadada Anita. Hivyo akaona mauaji hayo yana uhusiano wa karibu kwa kuwa na mkono wa mtu aliyekuwa akipanga mipango ile michafu!



    Hata hivyo kwa kujihami, Kachero Inspekta Malik alipiga simu katika Kituo cha Polisi Buguruni, na kuwajulisha juu ya tukio hilo. Haikuchukua muda mrefu, askari polisi wa doria waliokuwa kwa magari na miguu wakaanza kufanya msako wa nguvu kuwasaka watuhumiwa hao, Robi na Chogolo, ambao walikuwa wameshaondoka na kukimbilia kwenye ngome yao iliyoko Machimbo ya Mawe!



    Hivyo hawakupatikana!



    ********       



    MZEE Bwanga Feruzi alizipata habari za mtoto wake, Chikwala, kugongwa na gari eneo la Buguruni Sheli, katika Barabara ya Mandela, na maiti yake imepelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Yeye alikuwa ni baba yake mzazi  Chikwala, akiwa mtoto wa tatu, kati ya watoto wake sita aliowazaa.



    Baada ya kuzipata habari hizo, wanandugu walijikusanya na kupanga shughuli za msiba, zilizopangwa kufanyika nyumbani kwao, Yombo Dovya, Wilayani Temeke. Mzee Bwanga na wenzake wakaelekea katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ili kufanya taratibu za kuichukua maiti hiyo, lakini wakanyimwa na kuambiwa wawasiliane na Jeshi la Polisi kwanza kama maagizo yalivyokuwa yametolewa.



    Kachero Inspekta Malik Mkoba alipigiwa simu kesho yake asubuhi, wakati alipokuwa ameshafika ofisini kwake. Baada ya kuhakikisha ameshughulikia mafaili kadhaa, haraka sana alipanda gari lake na kuondoka kuelekea katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, kwa ajili ya kufanya mahojiano na mzee Bwanga, ili aweze kuupata ukweli wa kifo cha mtoto wake, Chikwala.



    Hatimaye Kachero Inspekta Malik alifika hapo hospitali na kulipaki gari lake katika sehemu ya maegesho. Akashuka na kuelekea katika ofisi ya Daktari Kenedy Mushumbuzi, ambaye ndiye anayeshughulika na maiti zenye utata. Baada ya kumwona daktari huyo, ndipo alipokutanishwa na mzee Bwanga Feruzi., aliyekuwa amefuatilia maiti ya motto wake, Chikwala.



    Mzee Bwanga alikuwa amevalia shati la rangi nyeupe iliyofifia karibu ifanane na rangi ya kahawia, na suruali ya rangi ya ugoro. Kichwani mwake alikuwa amevalia kofia ya baraghashia iliyofubaa, na pia iliyoweza kuonyesha nywele zake chache zilizokuwa na mvi chini yake. Chini miguuni alikuwa amevalia makubazi. Baada ya kukaa katika sehemu ya faragha, akamwita mzee huyo na kuanza kumhoji, ukiwa ndiyo utaratibu wa polisi.



    “Kwanza kabisa pole na msiba…” Kachero Inspekta Malik akamwambia mzee Bwanga.



    “Ahsante sana baba…ni kazi ya Mungu, kama alipanga mwanagu afe kwa kifo hicho, basi ndiyo yametimia…” mzee Bwanga akasema huku akionyesha mwenye huzuni sana.



    “Basi, mzee, kwa utaratibu wetu wa kipolisi, naomba kukuhoji maswali machache kwa vile marehemu kabla ya kupatwa na umauti nilimwona.” Kachero Inspekta Malik akamwambia mzee Bwanga.



    “Unasema ulimwona?” Mzee Bwanga akamuuliza huku akiwa bado amepigwa na butwaa!



    “Ndiyo, nilimwona,” Kachero Inspekta Malik akasema na kuongeza. “Yeye alikuwa amedhamiria kuniua mimi kwa risasi, lakini akanikosa, ndipo alipokimbia na hatimaye kugongwa na gari!”



    “Alitaka kukuua?” Mzee Bwanga akauliza huku amekunja sura yake!



    “Ndiyo…alitaka kuniua…”



    “Kukuua kwa sababu gani?”



    “Sijui, ndiyo maana nataka kukuhoji ili niweze kuujua ukweli, kwa kuijua historia ya marehemu kwa vile wewe ndiye mzazi wake.”



    “Sawa, baba, unaweza kunihoji tu…”



    “Naomba unieleze historia fupi ya marehemu mwanao…”



    “Kwa jina anaitwa Feruzi Chikwala Bwanga, ambaye nilimzaa miaka thelathini iliyopita huko Kisarawe. Amesoma mpaka kidato cha nne na baada ya hapo akajiajiri mwenyewe…”



    “Je, unajua kazi aliyokuwa anaifanya mwanao?”



    “Ndiyo…”



    “Ni kazi gani?”



    “Biashara…alikuwa anauza katika duka la vifaa vya ujenzi…”



    “Ni duka lake?”



    “Hapana, si lake…”



    “Ni la nani?”



    “Ni la tajiri mmoja ambaye hata mimi simfahamu…Chikwala alikuwa msiri sana!”



    “Je, ameoa?”



    “Hapana hajaoa…”



    “Anaishi wapi?”



    “Hata sijui…”



    “Yaani hujui mwanao anaishi wapi?”



    “Alikuwa msiri sana mtoto yule…oh!”



    “Basi, mwanao alikuwa jambazi!”



    “Unasema kweli?”



    “Ni kweli. Kwa sababu alitaka kuniua mimi kwa vile nafuatilia kesi fulani…”



    “Basi, mimi ndiyo kwanza nasikia hayo!”



    “Kama ndiyo kwanza unasikia, basi ujue hilo. Ni jambazi anayeshirikiana na huyo tajiri yake katika kuendesha vitendo viovu!”



    “Mh, mtoto ana laana huyo!” Mzee Bwanga akasema huku akitikisa kichwa chake!



    “Inawezekana ana laana, ndiyo maana yamemkuta hayo…” Kachero Inspekta Malik akamuunga mkono!



    “Sasa naomba utaratibu wa kuuchukua mwili wa marehemu…” mzee Bwanga akamwambia.



    “Sawa mzee, nakuruhusu kuuchukuwa mwili wa mwanao kwa ajili ya maziko….” Kachero Inspekta Malik akamwambia mzee Bwanga.



    “Sawa kijana wangu…” mzee Bwanga akashukuru na kwenda kuungana na wenzake kuendelea na taratibu za kuuchukua mwili wa marehemu.



    Kachero Inspekta Malik aliamua kuwaruhusu baada ya kuwasiliana na Mkuu wa Upelelezi, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, Alfred Gonzo. Hawakuona haja ya kuizuia maiti ile, kwani haikuwa na uwezo wa kusema!



    ********          



    JUMAPILI asubuhi majira ya saa tatu, kama kawaida ilimkuta Kachero Inspekta Malik akiwa eneo la Tabata Mawenzi katika nyumba aliyokuwa anaishi marehemu Anita. Ni katika juhudi za kuendelea na upelelezi wake, kwani alikuwa amemwahidi mama mwenye nyumba, Bi. Debora, kwamba angerudi tena kesho yake baada ya kuichukua ile albamu ya picha na picha mbili zilizokuwa kwenye bahasha ya khaki.



    Baada ya kusalimiana, Kachero Inspekta Malik alimwomba Bi. Debora waongee tena kuhusu marehemu Anita. Wakaongozana wote mpaka pembezoni mwa nyumba ile palipokuwa na bustani ya maua iliyokuwa na kivuli, pamoja na viti vya mianzi. Wakakaa pale huku wakitazamana tayari kwa mahojiano.



    “Kama nilivyokuelezea tokea jana, nimerudi tena katika upelelezi wangu…” Kachero Inspekta Malik akamwambia Bi. Debora.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Karibu sana baba…usijali sana…hapa ni nyumbani kwako…” Bi. Debora naye akamwambia.



    “Sasa kuna zile picha nilizochukua jana, ambazo nimezichunguza sana na kuona zina watu tofauti tofauti, akiwemo kijana mmoja. Ni kijana ambaye amepiga picha mara nyingi akiwa na marehemu Anita. Hebu chukua hii moja uniambie huyo kijana ni nani, au alikuwa na uhusiano gani na marehemu…” Kachero Inspekta Malik akasema huku akimkabidhi zile picha.



    Bi. Debora akazipokea picha hizo na kuanza kuziangalia kwa makini huku akitikisa kichwa na kusema kwa sauti ndogo, “Huyu kijana mimi namfahamu kwa sura tu, na ni mara nyingi alikuwa akimtembelea marehemu, jambo ambalo linaonyesha walikuwa na uhusiano wa karibu.”



    “Ina maana hukuwahi kumuuliza marehemu juu ya kijana huyo, akiwa ni mpangaji wako mliozoeana?” Kachero Inspekta Malik akaendelea kumuuliza Bi. Debora.



    “Hapana…sikuwahi kumuuliza, na wala sikupendelea kuingilia uhuru wa mtu. Maadam alikuwa ananilipa kodi yangu basi!”



    “Aisee, basi ulifanya kosa sana kumuuliza, ukiwa ni utaratibu wa mtu unayeishi naye. Kijana huyo ndiye angetusaidia katika upelelezi wetu, Jeshi la Polisi…” Kachero Inspekta Malik akamwam,bia huku akionyesha kusikitika kidogo.



    “Oh, masikini…” Bi. Debora akasema na kuendelea. “Kweli simfahamu kijana huyo, wala sehemu anayoishi hapa Dar au hata anakofanya kazi.”



    “Oohps! Basi iko kazi!” Kachero Inspekta Malik akasema huku akivuta pumzi na pia akimwangalia Bi. Debora.



    “Labda, ninachoweza kukusaidia mimi, labda uende kwa aliyekuwa rafiki yake wa karibu wa marehemu anayeitwa Getruda…”



    “Unasema rafiki yake wa karibu?”



    “Ndiyo.”



    “Na picha yake iko katika albamu hii?”



    “Ndiyo, ni huyu hapa…” Bi. Debora akaonyesha kwenye picha ambayo walipiga na Anita. “Ni wazi kwamba huyo kijana anatambulika na huyo rafiki yake, kwani mara nyingi walikuwa wanaongozana wote…”



    Kachero Inspekta Malik akamwelewa vizuri sana Bi. Debora, hivyo akamuuliza swali jingine. “Je, huyo rafiki yake, Getruda, anaishi sehemu gani hapa jijini Dar?”



    “Anaishi mtaa wa Moshi, Ilala, nyumba namba 003. Ni nyumba inayotazamana na Kanisa la Anglikana la Ilala, sehemu ambayo huwezi kupotea…”



    “Nashukuru sana mama. Mimi natoka na kama kuna mengine nitarudi tena unisaidie,” Kachero Inspekta Malik akamwambia.



    “Sawa baba…karibu tena…” Bi. Debora akasema.



    Kachero Inspekta Malik alipotoka pale Tabata Mawenzi, aliamua jambo moja tu! Ni kuelekea mtaa wa Moshi, Ilala, anapoishi mwanadada huyo anayejulikana kwa jina la Getruda. Alijua kuwa ni lazima atampata, kwani picha yake alikuwa nayo na hata sura yake aliweza kuikariri na kuiweka kichwani. Alijua fika kuwa, akikutana naye, anaweza kuambulia chochote cha maana, ambacho kitamsaidia kutatua kitendewili kinachomsumbua!



    ********      



    ALIFIKA katika eneo la  Bungoni, Ilala, kwa kuifuata Barabara ya Uhuru, ambayo kwa kiasi fulani ilikuwa na foleni ya magari iliyokuwa inakwenda mithili ya mwendo wa Kinyonga. Kachero Inspekta Malik Mkoba akapinda kulia kulia kuufuata mtaa wa Kasulu, kiasi cha mita ishirini hivi, halafu akapinda tena kushoto kuufuata mtaa wa Moshi huku akitupia macho namba za nyumba zilizokuwa mlangoni.



    Mbele kabisa Malik aliliona lile Kanisa la Anglikana, lililozungukwa na uzio wa ukuta. Ni kanisa lililojengwa zamani sana, ambalo lilikuwa katikati ya makazi ya watu. Alipotupa macho kushoto kwake, ndipo alipoiona ile nyumba namba 003 mlangoni, ambayo aliambiwa kuwa anaishi Getruda. Hivyo akasimamisha gari kando ya barabara, halafu akabakia humo ndani ya gari kwa muda wa dakika tano hivi, huku akichunguza eneo lile kwa ujumla kabla ya kushuka.



    Kachero Inspekta Malik akaiangalia nyumba ile ya kota iliyokuwa katikati ya nyumba nyingine zilizokuwa katika mtaa ule. Pale barazani alikuwepo msichana mmoja aliyekuwa anashona nguo kwa cherahani, akionekana kama ni mwenyeji katika nyumba hiyo. Pia, akauangalia mtaa ule wa Moshi kwa pande zote, unakoanzia na unakoishia, akaona kuna watu waliokuwa wanapita wakielekea katika shughuli zao, na magari vilevile yalikuwa yanapita ingawa hayakuwa mengi zaidi ya watu waliokuwa na ratiba zao eneo lile.



    Ndipo aliposhuka garini na kuiendea ile nyumba kwa mwendo wa taratibu hadi alipomfikia yule msichana aliyekuwa anashona nguo.



    “Hujambo binti?” Malik akamsabahi.



    “Sijambo…shikamoo…” msichana yule akaitikia huku akimwangalia na kuacha kushona nguo. Mkono mmoja akauacha juu ya Cherahani.



    “Marahaba binti…” Kachero Inspekta Malik akaitikia huku akimsogelea karibu.



    “Karibu kaka…”



    “Ahsante sana…wewe ni mwenyeji katika nyumba hii?” Malik akamuuliza.



    “Ndiyo, mimi ni mwenyeji, ninaishi humu ndani…” msichana yule akamjibu.



    “Vizuri, kama ni mwenmyeji, naona utanisaidia sana. Naomba kumuulizia dada mmoja anayeitwa Getruda, ambaye nimeelekezwa anaishi hapa…sijui nimemkuta?”



    “Hapana, dada Getruda hujamkuta,” msichana yule akamwambia huku akimwangalia kwa makini.



    “Aisee?”Malik akasema na kuendelea. “Amekwenda wapi?”



    “Amekwenda kusali kanisani.”



    “Kanisa hilo hapo?” Kachero Inspekta Malik akamuuliza akimaanisha lile Kanisa la Anglikana lililopo mtaa wa Moshi.



    “Hapana…amekwenda Kanisa Katoliki la Msimbazi, ambalo huwa anasali. Siyo hilo la Anglikana.”



    “Basi, nilikuwa na shida naye, kwani ni watu  tunaofahamiana. Lakini hakuna tatizo, namfuata hukohuko. Nitamsubiri mpaka atakapotoke…”



    “Haya kaka, karibu…”



    Kachero Inspekta Malik akajiondoa pale barazani na kuliendea gari lake, ambalo alipanda na kuodoka katika mtaa huo wa Moshi, kuelekea kwenye Kanisa Katoliki la Msimbazi, ambalo ni kanisa lililoko umbali wa mita mia moja kutoka barabara kuu ya Rashid Kawawa, eneo la Mchikichini. Pia, Kanisa hilo ambalo limejengwa miaka mingi na Wamishenari wa kikoloni, limezungukwa na uzio wa ukuta,  pamoja na femu za maduka ya biashara, na kwa mbele sehemu ya kuingilia pana na geti kubwa la chuma.



    Baada ya kufika katika eneo hilo, Kachero Inspekta Malik akalipaki gari lake katika sehemu ya maegesho mbele ya maduka yale, halafu yeye akajisogeza na kusimama karibu na lango kuu la kutokea pale kanisani. Aliamua kusimama eneo hilo ili ammsubiri Getruda atakapotoka, aweze kumtambua na kumfuatilia, na kwa sababu Malik alikuwa na picha yake, akajua asingepata shida ya kumtambua kwa kutumia ujuzi wa kipolisi kwa kuangalia.



    Baada ya kusimama hapo kwa muda wa nusu saa nzima, kengele ikagongwa kuashiria kumalizika kwa ibada, hivyo waumini walikuwa mbioni kutoka. Malik akakaa tayari kwa kukodoa macho yake kuelekea katika lango kuu la kutokea!



    ******** 



    GETRUDA alikuwa ni mmoja wa waumini wa mwanzo kutoka kanisani. Aliondoka huku akifuatana na waumini wenzake, akiwa na wazo moja tu, kwamba afike kwenye kituo cha daladala, apande daladala kuelekea nyumbani kwake, Ilala, akapumzike ukizingatia alikuwa amechoka kimwili na roho kutokana na matukio yale ya kutisha yaliyokuwa yametokea siku chache zilizopita.



    Muda wote nafsi yake ilikuwa ikimsuta Getruda kwa vile alikuwa ametoka kusali, lakini roho yake ikiwa chafu, imekaliwa na shetani, kwa yeye kuhusika kwa asilimia zote na kifo cha rafiki yake, Anita. Hakika mwenyezi Mungu kama angetaka kutoa adhabu kwake, angempatia muda wowote ule kwa vile alikuwa anamkejeli!



    Ndivyo alivyowaza!



    Hatimaye Getruda alitoka nje ya lango, na kuelekea usawa wa Barabara ya Kawawa kwa mwendo wa taratibu. Muda wote, Kachero Inspekta Malik aliyekuwa amekaa pale karibu na lango, aliendelea kukodoa macho yake, na kwa bahati nzuri aliweza kumwona Getruda akiwa katikati ya watu, ameshika biblia na kitabu cha nyimbo, akitembea mwendo wa taratibu na kuonyesha alikuwa na mawazo mengi sana.



    Kachero Inspekta Malik aliendelea kumkazia macho huku akimfuata nyuma. Getruda akavuka Barabara ya Kawawa hadi upande wa pili, kwani alitegemea kupanda daladala kurudi nyumbani kwake. Malik naye akavuka barabara hadi alipofika karibu yake, na kuendelea kumfuata nyuma huku akiusanifu mwili wake uliokuwa umesanifiwa vizuri na pia kutamanisha.



    Ni mwili ambao ulikuwa umefichwa ndani ya gauni la kitenge cha Wax, lilishonwa kulandana na mwili wake uliokuwa na umbile tata lililosumbua wanaume wengi, mmoja wapo akiwa John Bosho aliyeamua kumsaliti Anita!



    Si mchezo!



    Ni hadi walipofika kwenye kituo cha daladala zinazoelekea Kariakoo, Buguruni, Chang’ombe na kwingineko, ndipo Malik alipoamua kujaribu kumwita kwa vile alikuwa na uhakika kuwa ni yeye Getruda.



    “Dada Getruda…” Kachero Inspekta Malik akamwita kwa sauti ndogo kana kwamba walifahamiana.



    “Bee…” Getruda aliitikia kwa sauti ndogo yenye wasiwasi. Akageuka nyuma na kuangalia aliyemwita.



    Malik akamwonyeha ishara ya kumwita kwa mkono!



    “Unaniita mimi?” Getruda akamuuliza Malik.



    “Ndiyo, ninakuita wewe dada…” kachero Inspekta Malik akamwambia huku akimsogelea na kumtolea tabasamu laini. Baada ya kumfikia wakasalimiana na kupeana mikono. Wakati wote ule Getruda alikuwa bado na wasiwasi na kutomfahamu Malik.



    “Nafikiri hunifahamu dada…” kachero Inspekta Malik akamwambia Getruda.



    “Ni kweli…sikufahamu… ”



    “Vizuri,  kwa jina naitwa Maliki Mkoba …”



    “Malik …sawa kaka, unasemaje?”



    “Nina shida na wewe, na kwa ufahamisho zaidi, najulikana kama, Kachero Inspekta Malik Mkoba, nimetokea katika Kituo cha Polisi Buguruni, na safari yote hii nimekufuata wewe!”



    “Umenifuta mimi?” Getruda akamuuliza Malik huku wasiwasi ukiwa bado umeongezeka!



    “Ndiyo, nimekufuata wewe, ili nikuulize maswali machache….”



    “Maswali gani tena?”



    “Ni kuhusu kifo cha rafiki yako Anita, kwani nimeambiwa alikuwa mtu wako wa karibu. Tafadhali naomba unisaidie dada’ngu!”



    “Ah, polisi bwana…” Getruda akasema na kuendelea. “Ni nani aliyekwambia?”



    “Ni mama mwenye nyumba aliyokuwa anaishi kule Tabata, anayeitwa Bi. Debora. Natumaini na wewe unamfahamu sivyo?”



    “Ndiyo, Bi. Debora namfahamu. Na ni kweli marehemu Anita alikuwa rafiki yangu mkubwa,” Getruda akasema huku akilengwalengwa na machozi, ambayo yalikuwa yanadondoka!



    “Oh, pole sana, lakini naona hapa hapafai kuongelea mambo haya. Ni bora twende ofisini kwangu ili tuweze kuongea kirefu,”  Kachero Inspekta Malik akatoa pendekezo.



    “Ni sawa tu,” Getruda akakubali.



    “Basi, twende kwenye gari langu,” Kachero Inspekta Malik akamwambia.



    Wote wawili wakaongozana na kuelekea katika gari lake lililokuwa upande wa pili wa barabara, halafu wakapanda na kuondoka kuelekea katika kituo cha Polisi Buguruni. Kwa muda wote Getruda alijiona kama mtu aliyekuwa ndotoni, baada ya kutokewa na afisa yule wa polisi, anayepeleleza mauaji ya rafiki yake, Anita.



    Hakika Getruda alikuwa na wasiwasi hasa ukizingatia kwamba ni yeye aliyeingilia penzi la rafiki yake, baada ya kushawishiwa na John Bosho. Na pia, muuaji wa Anita alikuwa anamfahamu. Hata hivyo akajiapia moyoni kuwa asingemtaja muuaji wa Anita, Samson Kashaga, hasa ukizingatia alikuwa na mtandao mkubwa wa ujambazi!



            ********



    KITUO cha Polisi Buguruni kiliwalaki, ambapo Kachero Inspekta Malik Mkoba aliliingiza gari na kulipaki katika sehemu ya maegesho iliyokuwa upande wa pili wa kituo. Wakashuka na kuingia ofisini na kukaa, ilhali Getruda akiisikia harufu ya u-polisipolisi na hata bado akijisikia kama alikuwa katika ndoto fulani isiyoeleweka kabisa!



    Bila kupoteza muda Kachero Malik alifungua droo ya kabati na kutoa ile albamu ya picha pamoja na zile picha nyingine zilizokuwa ndani ya bahasha. Akampa Getruda ambaye alianza kuziangalia kwa makini, huku akifungua ukurasa mmoja baada ya mwingine.



    Akakubali kuwa alikuwa ameshaziona.



    “Vizuri kama umeangalia…sasa naomba unitajie jina la huyu kijana, sehemu anapoishi na  anapofanyia kazi…”  Kachero Inspekta Malik akmwambia Getruda kwa sauti ndogo ya kirafiki, ukizingatia aliuona ule wasiwasi aliokuwa nao!



    “Mh!” Getruda akavuta pumzi ndefu na kubaki akimwangalia Malik aliyekuwa anamsubiri amjibu swali lake alilomuuliza.



    “Mbona unaguna?”



    “Hapana…”



    “Hebu nieleze basi…”



    “Kijana huyu anaitwa John Bosho, na alikuwa mchumba wa Anita. Pia, walikuwa wamepanga kwamba wangeoana baadaye.”



    “Anafanya kazi gani?”



    “Ni mfanyabiashara maarufu sana hapa jijini Dar  es Salaam, na mikoani vilevile.”



    “Na anaishi sehemu gani?”



    “Anaishi Ukonga.”



    “Ukonga kubwa…sehemu ipi?”



    “Anaishi Ukonga Mombasa, nyuma ya Kambi Kuu ya Askari wa Kutuliza Ghasia Ukonga. Pale amejenga nyumba yake kubwa iliyoko kando ya reli ya kati, ni nyumba nzuri iliyozungukwa na uzio na inaonekana kwa uwazi zaidi….”



    “Unaweza kuniambia kuwa kabla ya kifo chake, marehemu alikuwa na mpenzi yupi zaidi ya John Bosho?”



    “Kusema kweli Anita alikuwa ni mtu msiri sana ingawa alikuwa ni rafiki yangu mkubwa. Na mambo mengine hakuniambia, hasa yanayohusu yeye binafsi.”



    “Je, wakati wa uhai wake alikuwa na maadui wangapi, au aligombana na nani?”



    “Anita aliishi vizuri sana na watu . hivyo sidhani kama alikuwa na maadui…” Getruda akamaliza huku akiuficha ukweli mwingine, ukizingatia hata yeye alichangia kifo cha Anita kwa kushirikiana kimapenzi na John Bosho. Lakini hayo hakuyasema!



    Ni hatari tupu!



    “Sawa Getruda, nashukuru sana kwa msaada wako wa maelezo mazuri uliyonipa. Kwa kiasi fulani yatanisaidia katika upelelezi wangu. Basi, twende nikurudishe nyumbani,” Kachero Inspekta Malik akamaliza huku akinyanyuka.



    “Sawa,” Getruda akasema huku naye akinyanyuka. Halafu wote wakatoka nje na kupanda gari la Malik. Safari ya kumrudisha nyumbani kwake, mtaa wa Moshi, Ilala, ikaendelea.



    Hatimaye baada ya nusu saa, Kachero Inspekta Malik alimfikisha Getruda nyumbani kwake, na yeye akageuza, akiwa amepanga kurudi nyumbani kwake, Shariff Shamba. Lakini wakati huo njaa ilikuwa inamuuma sana, ukizingatia alikuwa hajala kitu chochote tokea palipopambazuka kutokana na hekaheka zile zinamwandama. Siku zote anapoamua kufanya kazi, kamwe suala la chakula huwa analiweka kando kwanza!



    Hata hivyo wazo la kwenda nyumbani kwake aliliacha, hivyo akaamua kuingia katika hoteli Ubena  Resort, iliyoko eneo la Amana, Ilala, ili kujipatia chakula cha mchana. Ni hoteli nzuri inayotoa huduma nzuri ya chakula, hivyo baada ya kuingia na kukaa, akamwagiza mhudumu ampelekee chakula, wali kwa mchuzi na kuku wa kukaanga na bia moja aina ya Safari. Kwa vile huduma ilikuwa ni ya kuridhisha, mhudumu hakukawia kumpelekea kile chakula. Akaendelea kula taratibu, lakini kwa tahadhari ya hali ya juu.



    Ukweli ni kwamba, ilimbidi Malik ajilinde hasa ukizingatia hakujua adui yake alikuwa wapi, na upande gani! Hivyo akawa anatupa macho yake pande zote za hoteli hiyo bila mtu yeyote kumgundua, kwa vile yalikuwa macho ya kipelelezi. Watu wote waliokuwa wanaingia katika hoteli ile mchana huo, walionekana ni watu wa kawaida tu.



    Watu waliokuwa wanakwenda kula chakula hapo, aliwaona ni watu wa kawaida kabisa, kwa mujibu wa yeye alivyoweza kuwachunguza kwa kutumia uzoefu wake. Ni mara nyingi mtu anapokuwa adui yako ni lazima angekusaka huku akiwa na wasiwasi kidogo punde anapokuona kwa kugonganisha macho yenu. Sasa kati ya watu wote wale, hakukuwa na kitu hicho. Kila mmoja alikuwa na hamsini zake!



    ********



    GARI moja aina ya Toyota Corolla inayotoa huduma za teksi, ilisimamishwa nje ya Ubena Resort Hotel, kando ya Barabara ya Uhuru, eneo la Amana, Ilala. Baada ya kusimama, mlango wa nyuma ukafunguliwa, kisha akashuka mwanadada mmoja, mrembo wa nguvu, ambapo baada ya kushuka, alimlipa dereva fedha, na yeye akavuta hatua kuingia ndani ya hoteli hiyo.



    Ni muda mrefu ulikuwa haujapita tokea Kachero Inspekta Malik ameingia ndani ya hoteli hiyo na kuendela kula chakula. Ndipo alipoaingia mwanadada huyo, ambaye alikuwa na sifa zote za uzuri. Zaidi ya uzuri wake, pia, alionekana ana maringo, kwani alikuwa akitembea kwa mwendo wa Twiga.



    Kwa muda huo, mwanadada huyo alikuwa amevalia gauni la rangi ya pinki, fupi, lililoishia mapajani, na viatu vilivyofanana na lile gauni alilovaa, kwapani alikuwa ametundika mkoba mdogo, na moja kwa moja akaelekea kwenye meza ile aliyokuwa amekaa Malik. Baada ya kuifikia akavuta kiti kimoja na kukaa upande wa pili wa meza, na pia akaiweka simu yake  hapo juu ya meza.



    Harufu ya mafuta ya uzuri, ambayo hayakuleta kero puani, yalienea kote na kutoa burudani ya pekee, halafu baada ya kukaa, akauweka ule mkoba wake mezani na kuirekebisha ile nguo yake fupi iliyoacha wazi mapaja yake meupe yaliyonona!



    “Habari yako kaka…” mwanadada yule akamsalimia Malik.



    “Nzuri tu dada…” Kachero Inspekta Malik akaitikia huku akimwangalia kwa makini na kukubali ni kweli alikuwa mzuri na mrembo anayejipenda.



    “Samahani kaka, nimejikalia hapa, sijui kuna mtu mwingine?” Akamuuliza.



    “Unaweza kukaa tu, hakuna mtu,” Malik akamwambia huku akimshangaa! Ni kwanini akae pale, na siyo sehemu nyingine ndani ya hoteli ile!



    “Nashukuru…”



    “Du, imekuwa vizuri…utanisaidia kula, kwani chakula kingi hiki…” Kachero Inspekta Malik akamwambia kwa kumwonyesha ukarimu.



    “Nashukuru kaka’angu…nimeshaagiza chakula…” akajibu kwa sauti nyororo.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Muda gani, wakati umekuja sasa hivi tu? Tafadhali…”



    “Ndiyo, hapa hotelini nafahamika sana. Basi, wanaponiona huwa wanajua oda yangu.”



    “Aisee…kumbe ni mtu maalum.”



    “Ni kama hivyo kaka…”



    Baada ya muda mfupi, mwanadada huyo alihudumiwa chakula chake, ndizi kwa nyama, na bia moja aina ya  Castle ya baridi. Akaendelea kula taratibu. Pia, Malik naye akaendelea kula huku mawazo yakiwa mbali sana, hasa kuhusu mwanadada yule aliyekuwa pale, kwani ni mara nyingi alikuwa akijiepusha sana kumwamini mwanamke, hasa anapokuwa katika pilikapilika zake za kazi nzito ya upelelezi.



    Kuna wasiwasi kuwa, wanawake wengi huwa wanatumiwa na majambazi, wakitumika kama chambo kutokana na uzuri wao. Kachero Inspekta Malik akaukumbuka usemi ambao aliwahi kuambiwa na babu yake miaka mingi. Ni maneno machache, ambayo yalikuwa na ujumbe mzito uliosema:



     “…Mjukuu wangu, hivi sasa unakuwa mtu mzima. Kumbuka kwamba wanawake ni viumbe dhaifu, ingawa ni mama zetu waliotuzaa. Unaweza ukamkuta mwanamke mzuri, mfano wa Malaika; mwaenye sauti nzuri, nyororo na maneno mengi ya kuvutia. Lakini mara nyingine jihadhari na mwanamke huyo, kwa wakati mwingine anaweza kuwa na ulimi wenye sumu kali, inayoweza kukudhuru mara moja, ingawa siyo wote! Yakupasa kujihadhari!”



    Ndiyo. Kachero Inspekta Malik aliyakumbuka yale maneno punde tu alipokuwa amekaa sambamba na mwanadada huyo mwenye uzuri wa aina yake. Na wakati wakiendelea kula chakula, kimwana huyo ambaye walikuwa bado hawajafahamiana, alikohoa kidogo kusafisha koo. Halafu akanywa maji yaliyokuwa kwenye bilauri na kumwangalia Malik kwa macho malegevu! Mtego huo! Akawaza!



    “Samahani kaka…” mwanadada huyo akamwambia



    “Bila samahani…” kachero Inspekta Malik akamwambia..



    “Imekuwa kama bahati tumejikua tumekaa wote…ningependa tufahamiane, ikiwezekana jina lako, mahali unapopatikana na namba yako ya simu ya mkononi….” mwanadada huyo akaendelea kumwambia huku ameshika simu yake akiwa tayari kuingiza namba!



    Mbona haraka hivyo? Malik akajiuliza!



    “Mh!” Kachero Inspekta Malik akaguna. Akabaki ameshangaa sana juu ya mwanadada huyo mrembo kutaka kujua jina lake, kiundani zaidi, wakati walikuwa hawajafahamiana! Hakika alishindwa kutoa jibu!



    “Usiwa na wasiwasi…” mwanadada hyo akaendelea kumwambia na kuongeza. “Nimetokea kukupeda tu, ndiyo maana nikapenda kukaa na wewe. Unajua wewe ni kijana mtanashati uliyeumbika kiume. Lakini naomba usinielewe vibaya labda ukafikiri mimi ni malaya!”



    “Mungu wangu!” Malik akajisemea moyoni mwake! Hakumwelewa kabisa!



    “Upendo wangu kwako, ndio uliosababisha yote haya…” akaendelea kurindima. “Na pia nafahamu wazi kuwa utamaduni wetu ni vigumu mwanamke kumweleza mwanaume kuwa unampenda, zaidi ya kumwonyesha kwa vitendo…”



    “Huyu mwanamke vipi?” Kachero Inspekta Malik akaendelea kujiuliza!



    Hata hamu ya chakula ikamwisha!



    “Hata hivyo…” akaendelea mwanadada yule. “Uzalendo umenishinda mtoto wa kike…ndiyo maana nimekuomba usinielewe vibaya kaka, kwani sisi watu tuliotembea kidogo na kukutana na watu wengi, tumeshaivua aibu!”



    “Umeshamaliza?” Kachero Inspekta Malik akamuuliza!



    “Ndiyo…mimi nimemaliza. Nakusubiri tu wewe mtoto wa kiume!” Mwanadada yule akasema huku akijiamini sana!



    Kachero Inspekta Malik akawa na wasiwasi bado! Isije ikawa mwanadada huyo ni mtego wa majambazi, ukizingatia tokea jana alikuwa akiandamwa na kukoswakoswa na risasi ndani ya Kimicho Bar Buguruni, hivyo kwa kujihami akamwambia:



    “Unasikia dada…nimekuelewa sana. Hebu tufahamiane kwanza…wewe ni nani, jina lako, na unatika wapi, nafikiri huo ndiyo utaratibu.”



    “Ni kweli usemayo kakaangu…” mwanadada akasema huku akirembua macho yake makubwa mazuri na yenye mvuto.



    “Ok, unaitwa nani?”



    “Kwa jina naitwa, Helen Fataki….”



    “Vizuri sana. Ni jina zuri lenye mvuto, pia ni jina linalonikumbusha mbali sana!”



    “Ni kweli ee, basi nashukuru sana kwa kunisifia kaka…ni wachache sana hufanya hivyo.”



    “Ni wajibu wangu kukusifia Helen Fataki.”



    “Basi, tuendelee…” Helen Fataki akasema na kuendelea. “Mimi ni mfanyabiashara ninayeishi hapa jijini Dar es Salaam. Nakukumbusha tena kwamba nahitaji namba yako ya simu, kwani  najua tatizo unalolifuatilia, ambalo kwa namna moja ama nyingine ninaweza kukusaidia kulitatua. Kumbuka kwamba  mimi ni raia mwema!” Helen Fataki akamaliza kusema.



    “Tatizo linalonikabili?” Kachero Inspekta Malik akamuuliza.



    “Ndiyo, usiwe kama mtoto mdogo, mimi naelewa kila kitu, ndiyo maana nikakwambia mimi ni raia mwema, unanipata?”



    “Vizuri sana Helen, nimekuelewa….”



    “Nashukuru kama umenielewa.”



    Kachero Inspekta Malik  akamkubalia Helen baada ya kumsoma na kuona kwamba hakuwa na matatizo, na pia ni mtu ambaye alikuwa anajua kuwa yeye ni kachero ingawa hakuwa na namba zake za simu, ambazo ndizo zilikuwa kitu muhimu sana kwa upande wake. Hivyo akampa jina lake, namba zake za simu ya mkononi, na pia, Helen akampatia za kwake. Baada ya pale wakaagana kwa ahadi ya kuwasiliana zaidi kwa simu za mkononi, kila mmoja akaondoka.



    Kachero Inspekta Malik alielekea nyumbani kwake, Shariff Shamba, Ilala, huku akiwa na mawazo ya kujihami na adui zake waliojaribu kuzuia kazi yake aliyokuwa ameianza. Akaahidi kupambana nao kufa na kupona! Ni kiapo cha Ushindi!



    ********         



    MAWAZO mengi sana yalikuwa yamemtawala Getruda, mara baada ya kushushwa kwenye gari na Kachero Inspekta Malik, walipokuwa wametoka kwenye  Kituo cha Polisi Buguruni, katika mahojiano, alilekea nyumbani kwake kwa mwendo wa taratibu akiwaza jinsi Malik alivyoweza kugundua mapema kwamba walikuwa na uhusiano na marehemu Anita.



    Ukweli ni kwamba chanzo cha matatizo yote yale, yalikuwa yamesababishwa na yeye  mwenyewe, mara baada ya kumgeuka rafiki yake, Anita na kumchuka mchumba wake, John Bosho, na kushirikiana naye katika vitendo vya ngono. Na huko kukamfanya naye amgande kama Luba, mpaka yalipotokea mauaji hayo ya kumziba mdomo!



    Baada ya kufika nyumbani kwake alikopanga chumba, alimkuta yule msichana mdogo aliyekuwa anashona nguo pale barazani kwa cherahani, ambapo alimsabahi na kuanza kuingia ndani kwa hatua za kinyonge, lakini msichana yule akamwambia:



    “Habari za kanisani dada Getu…”



    “Nzuri tu Salma…za hapa..”



    “Hapa ni nzuri, lakini kuna mgeni wako alikuja hapa na kukuulizia…”



    “Mgeni wa aina gani? Mwanaume au mwanamke?”



    “Ni mwanaume, ambaye alikuja na gari ambalo alilisimamisha palee!”



    “Ameacha ujumbe?”



    “Hakuacha…hata hivyo nilimwambia kwamba umekwenda Kanisani, na yeye akasema kuwa anakufuata hukohuko, je, hujamwona?”



    “Ah, basi tu,” Getruda akamwambia, halafu akaingia ndani, kwani alikuwa ameshaonana na Kachero Inspekta Malik, ambaye mpaka muda ule hakuwa na hamu naye! Ni mtu ambaye aliona kwamba anataka kumwangamiza kabisa kama akiigundua ile siri nzito ya kifo cha Anita!



    Baada ya kuingia chumbani mwake, huku akiwa amesimama, Getruda akatoa simu yake ndani ya mkoba wake. Halafu akakaa kwenye egemeo la sofa, akiwa na nia ya kumpigia John Bosho. Ni juu ya kumjulisha mambo yalivyokuwa yanaendelea tokea walivyoachana juzi nyumbani kwake, Ukonga, alipokwenda kumtembelea baada ya kumwitakujadili hatima ya penzi lao.



    Akapiga simu ile upande wa pili ukasema:



    “Haloo…Getruda mpenzi…”



    “Oh, vipi mpenzi, hujambo?”



    “Mimi sijambo…sijui wewe!”



    “Hata mimi sijambo kiasi…nipe habari…”



    “Oh, amekuja!”



    “Amekuja nani?”



    “Askari mpelelezi.”



    “Mpelelezi yupi Getruda?”



    “Anajiita Malik Mkoba.”



    “Mh, Inspekta Malik Mkoba?”



    “Ndiye huyohuyo!”



    “Unasema amekuja hapo nyumbani?”



    “Ndiyo…amekuja hapa nyumbani na kunikosa, halafu akanifuata Kanisani na kuanza kunihoji kuhusu wewe, kama nakufahamu.”



    “Ni nani aliyemweleza?”



    “Ameelekezwa na mama mwenye nyumba aliyokuwa anaishi Anita kule Tabata…”



    “Aisee…” John Bosho akasema. “Kumbe yule mama ni mtu mshenzi sana!”



    “Usiseme hivyo John, yule mama amehojiwa tu. Lakini si unajua polisi walivyo?”



    “Sasa baada ya kukuhoji ukamwambia nini kuhusu mimi?”



    “Ilinibidi nimwambie…” Getruda akasema na kuendelea. “Sikuwa na jinsi, kwani alivyokuja hapa alikuwa na habari kamili, pamoja na picha zetu wote. Wewe, mimi na marehemu Anita!”



    “Mama yangu! Amezipata wapi?”



    “Bila shaka amezichukua chumbani kwa Anita baada ya kufanya upekuzi.”



    “Mh!” Akaguna John. “ Ulimweleza juu yangu?”



    “Basi, ndiyo hivyo John. Nilimwelewa, lakini sikumwambia kwamba wewe ndiye muuaji. Nimemtambulisha kama mfanyabiashara mkubwa.”



    “Oh, vizuri sana…sasa unanipa ushauri gani?”



    “Nilikuwa nakufahamisha tu, ili ujihami!”



    “Kujihami ni muhimu sana. Hivyo basi, kuanzia sasa, tena leo hii, fanya hima uje hapa nyumbani kwangu Ukonga, ili ujifiche. Kwa mimi ninavyowajua polisi, anaweza akarudi tena kukupeleleza ili kutaka sifa!”



    “Sawa, nafungasha nguo zangu. Nitakuja huko muda siyo mrefu, kwani nimeshaanza kuingiwa na wasiwasi…”



    “Na ukitoka hapo usimuage mtu yeyote kuwa unaelekea wapi! Iwe siri yako! Tafadhali zingatia!”



    “Sawa, nitazingatia…”



    “Ok, bai…”



    Wakamaliza kuwasiliana.



    Kuanzia muda ule Getruda hakupoteza muda, akaanza kukusanya nguo zake muhimu za kubadili, ambazo alizitia ndani ya begi dogo. Pia, akachukua vikorombwezo vingine vingi ambavyo aliona vingemsaidia katika safari yake ile ya kuyakimbia makazi yake pasipo kupenda! Baada ya kumaliza kukusanya aliyoona vinamfaa, akaamua kujipumzisha kwenye kochi kubwa akingali bado anasumbuliwa na mawazo.



    Ni mawazo ambayo yalimfanya hata asisikie njaa kutokana na kasheshe lile lililoanza kufukuta kichinichini. Ama kweli pale ndipo alipoamini kuwa mkono wa dola ni mrefu, usioweza kukwepeka kamwe! Kwa mbali akawa anaendelea kuujutia ule uamuzi wake wa kukubali kurubuniwa na John Bosho, kwa ajili ya fedha! Hata hivyo kuwaza sana halikuwa suluhisho la kutatua tatizo lake. La muhimu ilikuwa ni jinsi ya kupanga kuepukana nalo kwa gharama yoyote!



            ********



    ILIPOTIMU saa kumi na moja za jioni, Getruda akaamua kuodoka pale nyumbani kwake kuelekea Ukonga. Ingawa John alimwambia asiage mtu yeyote, lakini hakufanya hivyo, aliwaaga wapangaji wenzake na kuwadanganya kwamba alikuwa anakwenda Sinza kwa shangazi yake. Hata hivyo, hakuna hata mtu mmoja aliyemhoji zaidi ya kumtakia safari njema. Getruda akakodi teksi iliyokuwa inapita katika mtaa ule wa Moshi, na kumwambia dereva ampeleke Ukonga.



    Safari ikaendelea kwa mwendo wa wastani. Dereva akaendelea kupangua gea na kukanyaga mafuta hadi walipofika Ukonga Mombasa. Nusu iliyobaki akaamua kutembea kwa miguu, kuelekea nyumbani kwa John Bosho, kwa kukatiza pembezoni mwa Kambi ya Askari wa Kutuliza Ghasia, na kutokeza relini ilipo nyumba inayomilikiwa na John Bosho.



    Baada ya kufika  kwenye makazi ya John Bosho, Getruda aliingia kama mwenyeji, mara baada ya kuruhusiwa na mlinzi wa kimasai aliyekuwa analinda hapo getini. Alipoingia ndani, alimkuta John Bosho akiwa amekaa sebuleni katika sofa za gharama akiangalia runinga. Na kama ilivyo ada mbele yake kwenye meza ndogo, ulikuwepo mzinga wa Konyagi aliokuwa anakunywa taratibu kuisukuma wikiendi.



    “Oh, karibu sana Getu…” John Bosho akasema huku akinyanyuka kumpokea lile begi dogo. “Karibu…”



    “Ahsante, nimekaribia…” Getruda akasema huku akikaa kwenye sofa, na pengine kumkazia macho John. “Safari gani ya kupewa pole?”



    “Ni lazima nikupe pole kwa sababu ni safari ambayo ulikuwa hujaipangilia…”



    “Ahsante…nimepoa…”



    John Bosho na Getruda walikaa pale sebuleni huku wakiongea hili na lile, hatimaye John akatoa wazo kuwa siku ile ya Jumapili watoke kidogo nje ya nyumbani, ili wakale chakula cha usiku na pia vinywaji. Getruda ambaye kwa muda mwingi alikuwa ni mtu wa kukubali tu, hakupinga wazo lile, akakubali kwenda kule alipoamua kwenda . Hivyo basi, wakatoka nje wakiwa kama wapenzi wawili huku wameshikana mikono, wakapanda ndani ya gari na kuodoka eneo hilo huku wakimwacha yule mlinzi wa kimasai akilinda eneo la nyumba.



    “Huyu mlinzi wa kimasai mwisho wake wa kazi ni leo…simtaki tena!” John Bosho akamwambia Getruda.



    “Kwa nini humtaki?” Getruda akahoji.



    “Nimemshtukia…hawezi kutunza siri punde atakapohojiwa na polisi…”



    “Kwa hivyo umempata mwingine?”



    “Ndiyo. Nimempata kutoka kwenye kampuni ya ulinzi ya binafsi, ambao nimeshaandikishiana nao mkataba. Ataanza kazi kesho, na huyu namlipa haki yake aende sehemu nyingine!”



    “Ni sawa kama umeamua hivyo…” Getruda akamuunga mkono.



    “Ni uamuzi wa busara!” John akamaliza kusema huku akiongeza mwendo wa gari wakiifuata Barabara ya Pugu, kuelekea Gongo la mboto.



    John Bosho aliamua kwenda kuburudika katika sehemu tulivu ya Mangi Villa Bar, ikiwa ni sehemu iliyotulia sana na pia burudani ya muziki wa Zilipendwa ulipatikana. Kama kawaida Getruda alikubaliana naye hadi walipofika, akaliegesha gari sehemu ya maegesho palipokuwa na magari mengine. Halafu wakashuka na kwenda kukaa kwemye sehemu nzuri iliyokuwa nje yenye upepo.



    Baada ya kukaa, vyakula navinywaji na kuendelea kula na kunywa, na pia wakiendelea na maongezi yao mengi yakiwepo ya yeye John kutaka kumwoa Getruda, ili aje kuwa mke wake atakayemzalia watoto. Hata hivyo pamoja na kuimbiwa kawimbo hako ka mapenzi, Getruda alikuwa mbali sana kimawazo dhidi ya mtu huyo katili!



    Ni hadi ilipotimu saa tano za usiku, waliamua kuondoka hapo Mangi Villa Bar, kurudi nyumbani wakiwa wamechangamka vya kutosha. Muda wote huo John Bosho alikuwa na hamu kimapenzi na Getruda, bila kuwazia ule unyama alioutenda kwa rafiki yake, Anita, na isitoshe hata wiki moja ilikuwa haijaisha!



    *********      



    JUMATATU asubuhi kunako majira ya saa moja na nusu, ilimkuta Kachero Inspekta Malik alikuwa ofisini kwake akichapa kazi, ukizingatia alikuwa na mafaili kadhaa ya kuyashughulikia. Alikuwa amepanga kwamba achape kazi mpaka saa tisa za alasiri, halafu ndiyo aende nyumbani kwa John Bosho, Ukonga, akaendelee na upelelezi wake aliouanza.



    Mawazo yakiwa yamezama ndani ya faili moja, mara simu yake ya mkononi iliyokuwa kando ya meza ikaita. Akaichukua na kuangalia namba za mpigaji, ambazo zilionyesha ni za mwanadada Helen Fataki, ambaye walikuwa wamekutana naye jana yake na hatimaye kupeana namba za simu zao za mkononi.



    “Haloo…Helen…Malik hapa…” Kachero Inspekta Malik akamwitikia.



    “Ndiyo mimi Helen Fataki naongea…vipi hali…”



    “Hali nzuri, habari za tokea jana.”



    “Habari ni nzuri.”



    “Nashukuru sana kwa kunikumbuka kwa simu asubuhi hii Helen…” Malik akamwambia.



    “Nami nashukuru. Samahani kwa usumbufu, najua uko bize sana.”



    “Ni kweli Helen. Si unajua kazi zilivyotutinga? Nimeelewa si mchezo!”



    “Ok, sasa kuna la maana nataka kukueleza. Hivyo naomba jioni tukutane sehemu gani kwa maongezi zaidi?”



    “Naomba upange wewe sehemu ya kukutana Helen…” Malik akamwambia.



    “Tukutane Sarova Pub, hapo Buguruni…”



    “Sarova Pub iliyoko jirani na Kimicho Bar?”



    “Ndiyo.”



    “Kwa nini umeamua tukutane hapo?”



    “Ni sehemu ambayo kazi yetu inaanzia hapo. Nataka tukutane, ili nikupe michapo juu ya kazi unayoifuatilia. Ninarudia kuwa ni muhimu!” Helen Fataki akasisitiza!



    “Muda gani?”

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Saa moja za usiku…samahani kwa usumbufu…”



    “Bila samahani Helen…nitafika…”



    Baada ya kumaliza kuwasiliana, Kachero Inspekta Malik akaendelea kuchapa kazi, ambapo kwa siku ile nzima aliamua kushinda ofisini hadi ilipotimu saa tisa na nusu, ndipo alipomaliza kazi na kufunga ofisi. Kama alivyokuwa amepanga, akapanda gari na kuelekea Ukonga, nyumbani kwa John Bosho kufuatilia nyendo zake ukizingatia alikuwa bado hajamfahamu. Kwa vile Getruda alishamwelekeza nyumbani kwake, basi akajua asingepotea, ataifuata ramani iliyoko kichwani mwake!



    Ili asishtukiwe, kachero Inspekta Malik alilipaki gari lake eneo maarufu la Ukonga Mombasa, ambayo ni sehemu yenye pilikapilika nyingi za watu. Halafu akachepuka kwa miguu na kukatiza vichochoro hadi alipotokeza upande wa pili sehemu ya relini kama alivyokuwa ameelekezwa. Baada ya kutokea eneo lile, akaanza kuchunguza nyumba ya John, ambayo hakupata shida kuiona ikiwa imezungukwa na ukuta madhubuti, na mbele kukiwa na geti kubwa la chuma.



    Akaamua kuiendea ile nyumba kana kwamba alikuwa mwenyeji na getini akamkuta mlinzi wa kampuni ya binafsi akiwa amesimama kwa ukakamavu na makini kwa lindo lake. Mlinzi huyo ndiye yule aliyekuwa amewekwa siku ile, mara baada ya John kuamua kumwachisha kazi yule mlinzi wa kimasai aliyekuwa mwanzo, kwa kile alichokiita kutomwamini kujibu maswali ya polisi walioanza kumfuatilia.



    Kwa wakati huo, mlinzi huyo wa kampuni binafsi alikuwa amevalia sare zake za rangi ya bluu na michirizi ya njano. Akawa anamwangalia Malik alivyokuwa anamwendea pale aliposimama.



    “Habari za kazi!” Kachero Inspekta Malik akamsalimia baada ya kumfikia.



    “Nzuri tu…nikusaidie…” mlinzi yule akaitikia huku akimkagua Malik, kuanzia juu hadi chini, ukizingatia masharti aliyokuwa amepewa na John Bosho. Ni kujihadhari na watu waliokuwa wanafika pale kumuulizia!



    “Nisaidie ndugu yangu. Naulizia kwamba hapa ni nyumbani kwa mfanyabiashara, John Bosho?” Kachero Inspekta Malik akamuulizia huku amemkazia macho yake ya kipolisi, ambayo mlinzi aliyakwepa!



    “Hukukosea…ndiyo penyewe!” Mlinzi akasema.



    “Sijui nimekuta?”



    “Ndiyo…umemkuta…”



    “Basi, nina shida naye…”



    “Una ahadi naye?”



    “Sina ahadi naye,” Kachero Inspekta Malik akamwambia. “Ninataka kumuona tu, wala sikuwa na miadi…”



    “Aisee…” mlinzi yule akasema huku akionyesha kama vile anasita. Hakuwa tayari kumruhusu kwa jinsi alivyoelekezwa na John Bosho.



    “Kwani kuna masharti ya kumwona?”



    “Ndivyo alivyoamua bosi mwenyewe!”



    “Mjulishe bosi wako! Mweleze kwamba kuna mgeni anataka kuonana naye. Kuna jambo la muhimu.”



    “Sawa,” mlinzi yule akasema huku akiona ilikuwa ni adha imeanza!



    Mlinzi akachukua simu yake ya mkononi na kubonyeza namba kumpigia John Bosho aliyekuwa ndani. Simu ikaanza kuita na mlinzi kuanza kuisikiliza huku ameyakodoa macho yake makubwa kwa Malik. Upande wa pili wa simu, John akamwuliza kwa hasira kidogo!



    “Unasemaje?”



    “Kuna mgeni bosi!”



    “Mgeni? Mwanaume au mwanamke?”



    “Mwanaume…”



    “Umemuuliza jina lake?”



    “Hapana…sijamuuliza bosi.”



    “Ok, mruhusu aingie…”



    “Sawa bosi…” mlinzi yule alikasema huku akiendelea kumwangalia Malik, ambaye alikuwa ameshayagundua yale maongezi waliyokuwa wanaongea! Halafu akamwambia.



     “Amesema uingie…”



    “Ina maana kuna masharti ya kumwona?”



    “Ndivyo alivyopanga yeye mwenyewe…na isitoshe mimi nimeanza kazi leo!” Mlinzi yule akasema huku amechukia!



    Hata hivyo Kachero Inspekta Malik hakumsemesha tena, isipokuwa aliamua kuingia ndani kwa kupenya katika mlango mdogo uliokuwa pale getini, na kutokeza ndani ya nyumba ile ya kifahari iliyokuwa na bustani nzuri na ya kupendeza. Baada ya kuingia tu, akamwona Getruda akiwa amesimama nje ya kibaraza cha nyumba, na baada ya kumwona Malik akashtuka na kujikuta akisema kwa sauti ya kujilazimisha:



    “Oh, karibu Inspekta Malik…”



    “Ahsante sana…” Kachero Inspekta Malik akaitika na kushangaa kumkuta Getruda katika nyumba ile, wakati ilikuwa ni ya John Bosho, aliyekuwa mchumba wa marehemu Anita! Ambaye ni rafiki yake mkubwa Getruda!



    “Ooohps!” Getruda akavuta pumzi ndefu na kuzishusha kwa nguvu!



    “Vipi Getruda…mbona uko hapa?” Kachero Inspekta Malik akamuuliza baada ya kumkuta pale, kwani hakutegemea!



    “Kwani vipi?” Getruda naye akamuuliza



    “Nauliza hivyo kwa sababu hapa ni nyumbani kwa shemeji yako. Isitoshe rafiki yako Anita amefariki, au sivyo?”



    “Nimekuja kumsalimia shemeji yangu John, kwani kuna ubaya wowote?”



    “Hakuna ubaya,” Kachero Inspekta Malik akasema kwa kumtoa wasiwasi Getruda. Hata hivyo akagundua kuwa amemsaliti mwenzake kwa kuanzisha uhusiano usiofaa, hususan wa kimapenzi na John.



    “Vipi, John nimemkuta?”



    “Umemkuta, yuko ndani…”



    “Vizuri sana…imekuwa bahati sana…”



    “Bahati gani?” Getruda akamuuliza.



    “Kumkuta, kwani ni mtu muhimu sana kwa wakati huu!”



    “Karibu…utamkuta tu, kajaa tele ndani.”



    Kachero Inspekta Malik na Getruda wakaingia ndani huku Getruda ametangulia, na Malik akimfuata nyuma. Baada ya kuingia pale sebuleni, wakamkuta John amejaa tele amekaa kwenye sofa, na alipomwona Malik, akanyanyuka na kujifanya kumchangamkia kwa kumkaribisha kwa ukarimu.



    “Oh, karibu mgeni…karibu sana…”



    “Ahsante…nimekaribia…” Malik akasema huku akijiandaa kukaa kwenye sofa dogo.



    Kachero Inspekta Malik akakaa kwenye sofa lile dogo, moja kati ya yale matatu ya thamani yaliyokuwa katika sebule ile kubwa iliyosheheni samani.



    “Karibu na ujisikie uko nyumbani…” John Bosho akaendelea kumwambia Malik.



    “Ahsante, na nimeshakaribia…” Kachero Inspekta Malik akasema huku akiangaza macho yake pande zote za sebule ile nadhifu.



    Ukimya mfupi ukatawala kwa muda pale ndani, baina ya watu wale, Kachero Inspekta Malik, John Bosho na Getruda, kila mmoja akitegea atakayeanza mazungumzo!



    ********



    TOKEA mwanzo John Bosho  alishagundua kuwa aliyefika pale nyumbani kwake, Ukonga, alikuwa ni Kachero Inspekta Malik Mkoba, aliyekuwa anafuatilia kadhia ile ya mauaji ya Anita, aliyemuua yeye mwenyewe. Ndipo alipomwambia Getruda akampokee kule nje, ingawa yeye Getruda hakujua kama ni Malik, zaidi ya mgeni wa kawaida tu, ambao huwa wanafika mara kwa mara kumtembelea. Kumbe haikuwa hivyo!



    Basi, baada ya Getruda kutoka nje tu, ndipo yeye John alipoingia chumbani kwake, ambapo  alichukua bastola yake iliyokuwa imejaa risasi, halafu akaichomeka kiunoni upande wa nyuma, akaifunika na fulana aliyokuwa amevalia. Alipomaliza kuihifadhi, ndipo alipotoka pale chumbani na kurudi sebuleni alipokuwa amekaa mwanzo, na kuendelea kuangalia runinga huku amechukia kwa kile kitendo cha kufuatwafuatwa! Pia, akawa anamsubiri mgeni wake kwa hamu!



    Wakati John Bosho akimkaribisha Malik, Getruda alibaki amesimama, akisubiri kumkarimu mgeni yule, japo kwa kinywaji anachopendelea. Na muda huohuo, John akamkabidhi Getruda kipande cha karatasi kilichokuwa na ujumbe mfupi uliosomeka hivi “Ingia chumbani, fungua droo, chukua ‘Sumu ya nyongo ya Mamba,’ mtayarishie mgeni juisi ya maembe. Tafadhali tekeleza!”



    Baada ya kuuchukua ule ujumbe, Getruda aliondoka na kuelekea ndani chumbani alipoelekezwa kuwa kuna ile sumu kali, ili amtayarishie mgeni wao juisi.



    “Ndiyo bwana, mimi naitwa Kachero Inspekta Malik Mkoba…nimetokea katika kituo cha Polisi, Buguruni,” Kachero Inspekta Malik akajitambulisha kwa John Bosho.



    “Nashukuru kwa kukufahamu, karibu sana,” John Bosho akamwambia Malik.



    “Samahani sana kwa kuingilia mapumziko yako ya jioni…”



    “Bila samahani.”



    “Natumaini kuwa wewe ni John Bosho, maana sikufahamu…”



    “Naam, ndiyo mimi…”



    “Ok, mimi nimekuja hapa kwako kwa ajili ya upelelezi wa kifo cha marehemu Anita, kwa vile nasikia alikuwa mchumba wako.”



    “Ni kweli afande, Malik, kabla ya kifo chake, alikuwa ni mchumba wangu…”  John Bosho akasema huku akiwa na wasiwasi.



    “Sasa ndugu John, kama Anita alikuwa ni mchumba wako wakati wa uhai wake, mbona kwenye msiba wake au siku za mazishi hukufika?”



    Swali lile likawa gumu kwake. Akanyamaza kimya!



    Halafu Malik akaendelea “…Yaani hukuonekana kabisa hata sura yako!”



    “Ah, unajua…nili…kuwa sababu…” John Bosho akaendelea kujikanyaga.



    “Narudia tena…hivi ina maana kweli Anita alikuwa mchumba wako, halafu wewe usiende kwenye msiba wala mazishi yake?” Kachero Inspekta Malik akaendelea kumhoji.



    “Nilikuwa ‘Bize’ sana…hapana…unajua mimi nilisafiri…”  John akazidi kujichanganya! Hakika alikuwa amekumbana na maswali ya kikachero, ambayo hakujiandaa kuyajibu.



    “Hivi John, unaweza kuwa ‘Bize’ mpaka ukashindwa kuhudhuria mazishi ya mchumba wako?”



    “Mh,” John Bosho akajibu kwa kuguna.



    “Enhe, hivi na huyu mwanadada aliyenipokea hapa ni nani kwako?” Kachero Inspekta Malik akaendelea kumuuliza swali jingine, ambalo lilikuwa ni mtego, kana kwamba alikuwa hamfahamu Getruda!



    “Huyu ni mchumba wangu Getruda…” John Bosho akasema bila kuwa na wasiwasi wowote!



    “Unasema ni mchumba wako?”



    “Ndiyo, ni mchumba wangu mpya!” John Bosho akasema na kuongeza, “Vilevile alikuwa ni rafiki wa Anita.”



    “Kwa hiyo huoni ubaya wowote kumwoa msichana huyu, wakati alikuwa rafiki wa mchumba wako, marehemu Anita?”



    “Kwa hilo mimi sioni ubaya wowote. Isitoshe kila mmoja ana nafasi yake!” John Bosho akajibu kijivumi, huku amechukia! Hata hivyo akamezea, na ukimya ukatawala kwa muda kila mmoja akitafakari lake kichwani!



            *********

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    AKIWA katika hali ya sintofahamu, baada ya kuuchukua ule ujumbe kutoka kwa John Bosho, Getruda alikuwa ameshaondoka na kuelekea ndani chumbani alipoelekezwa kuwa kuna ile sumu kali, ili amtayarishie mgeni wao juisi. Na kweli alipoingia humo chumbani, alifungua droo na kuitoa ile sumu iliyokuwa katika hali ya unga mweusi ndani ya pakti maalum ya nailoni iliyofungwa madhubuti. Alipoichukua, akaenda nayo jikoni na kuichanganya katika juisi ya maembe iliyokuwa ndani ya friji.



    Sumu hiyo alikuwa ameiweka ndani ya bilauri ya Kachero Inspekta Malik, na kuijaza juisi ndani yake. Alipomaliza kuiandaa akaipeleka mezani ikiwa ndani ya jagi la kioo, pamoja na bilauri tatu kubwa. Hakika ilikuwa ni juisi iliyotamanisha kuinywa, kiasi kwamba hakuna mtu yeyote ambaye angeacha kuitamani na kuacha kunywa. Ilikuwa ya mchanganyiko wa rangi ya njano iliyokolea.



    Hivyo basi, Getruda alimmiminia Malik hiyo juisi na kumsogezea stuli iliyoundwa kwa kioo, ikiwa ni moja kati ya stuli nne zilizokuwa pale sebuleni pamoja na meza yake. Ile bilauri ya juisi akaiweka juu ya stuli hiyo kwa heshima ya kuvunja goti kwa kuinama kidogo, na kumwambia:



    “Karibu juisi…”



    “Ahsante sana…” Kachero Inspekta Malik akasema huku akiitamani ile juisi ya maembe kwa mwonekano wake.



    “Karibu juisi ndugu, Malik…” John Bosho  akamwambia huku yeye akiichukua bilauri yake na kuanza kunywa taratibu ili kumwondoa wasiwasi!



    “Ahsante sana,” kachero Inspekta Malik akasema na kuinyanyua ile bilauri kubwa tayari kwa kuinywa, na tayari alikuwa ameshaisogeza mdomoni!



    Getruda aliyekuwa akimwangalia kwa makini, aliyafumba macho yake wakati Malik alipokuwa anaipeleka bilauri ile mdomoni mwake. Kwa vyovyote alijua kuwa muda wowote ule atakuwa mfu, kitu ambacho kilimwogopesha sana!



    Lakini kabla Malik hajainywa ile juisi, simu yake ya mkononi iliita hapohapo! Halafu akaitoa mfukoni mwake na kuangalia namba za mpigaji, ambapo ilionyesha ni za Mkuu wa Upelelezi Kituo cha Polisi Buguruni , Mrakibu Mwanadamizi wa Polisi, Alfred Ganzo, ndiye aliyekuwa akimpigia muda ule. Hivyo Malik akataka kuirudisha ile bilauri mezani huku bado akiiangalia ile simu iliyokuwa inaita mkononi mwake!



    Hata hivyo kwa bahati mbaya, bilauri ile iliteleza katika stuli ile ya kioo na kudondoka chini kwa kujipigiza kwenye sakafu ya tarazo, na bilauri ile ikavunjika na juisi yote kumwagika! Hakika ilikuwa ni bahati ilioje, kwani hakuwahi hata kuionja hata kidogo!



    “Oh!” Kachero Inspekta Malik akaguna huku akiitazama ile bilauri iliyokuwa imevunjika.



    “Ah, bahati mbaya!” John Bosho akasema huku akishangaa!



    “Mungu wangu!” Getruda akaishia kusema hivyo!



    “Ngoja niliisikilize simu…”  Kachero Inspekta Malik akasema. Hakujali, akanyanyuka na kujisogeza pembeni kabisa karibu na mlango wa kuelekea kwenye korido. Akaanza kuisikilize ile simu iliyokuwa bado inaita.



    John Bosho na Getruda walibaki wanaangalia kwa mshangao na hamaki! Hawakujua kingetokea kitu kama kile, kwani walitegemea angeinywa ile juisi iliyoachanganywa na sumu ya nyongo ya Mamba! Afe, wakamzike shambani, mchezo kwisha!



    “Afande…naomba maelekezo…” Kachero Inspekta Malik akasema kwa sauti ndogo.



    “Malik uko wapi?”  Alfred Gonzo akamuuliza.



    “Niko hapa Ukonga, afande…”



    “Si unajua kwamba hatujaonana kabisa?”



    “Ni kweli afande, hatujaonana…niko kwenye pilikapilika za upelelezi.”



    “Unafuatilia lile tukio la mauaji siyo?”



    “Ndiyo, afande!”



    “Umefikia wapi mpaka muda huu?”  Alfred Ganzo akamuuliza na kuendelea. “Maana Mkuu wa  Upelelezi Kanda Maalum, anaulizia…”



    “Afande, ninaendelea vizuri, lakini siwezi kukuelezea kwenye simu…”



    “Kwa hivyo?”



    “Nakuletea taarifa…sijui utakuwepo ofisini?”



    “Niende wapi na mimi nasumbuliwa? Njoo nakusubiri…”



     “Sawa afande, nakuja kukupa taarifa za upelelezi wangu..”



    “Ok, nakushukuru…”



    Baada ya kumaliza kuwasiliana na mkuu wake,  Kachero Inspekta Malik aliwageukia John na Getruda waliokuwa bado wanaagaliana, kisha akamwambia kwa sauti ndogo:



    “Jamani mimi nashukuru kwa karibu yenu, lakini nahitajika ofisini mara moja. Lakini nitarudi baadaye…”



    “Oh, ngoja basi nikumiminie juisi nyingine…” Getruda akamwambia baada ya kuona mpango wao haujakaamilika!



    “Nashukuru sana…nitakunywa siku nyingine!” Kachero Inspekta Malik akasema huku akiona kwamba alikuwa anapoteza muda, ukizingatia alikuwa anasubiriwa na mkuu wake wa kazi!



    Kachero Inspekta Malik akatoka kwa hatua za haraka huku akisindikizwa na John Bosho, huku nyuma wakifuatiwa na Getruda hadi walipofika nje ya geti. Malik akachanganya hatua kuelekea eneo la Ukonga Mombasa, alipokuwa ameliacha gari lake, wenyewe wakarudi ndani huku wameghadhibika!



    Kachero Inspekta  alipoondoka pale nyumbani kwa John Bosho, wala hakuwa na habari kwamba alikuwa ametiliwa sumu kwenye juisi ili afe! Hakuwa na wasiwasi kuwa John angeweza kumdhuru!



    Alijiamini sana!



          ********



    WOTE wawili, John Bosho na Getruda waliporurudi ndani, yeye John alifura kwa hasira na kubaki akizunguka pale sebuleni kama mtu aliyechanganyikiwa. Ina maana windo lake limefanikiwa kumponyoka? Tena ndani ya himaya yake? Hakutegemea kabisa!



    “Mshenzi sana huyu kachero! Atanitibulia mipango yangu!” John Bosho akasema kwa hasira!



    “Ukweli ni kwamba ana bahati sana!” Akaongeza Getruda.



    “Sikubali!” John akasema kwa hasira!



    “Hukubali nini?” Getruda akamuuliza.



    “Yaani aniponyoke hivihivi?”



    “Sasa unatakaje?”



    “Mimi namfuata kummaliza!” John Bosho akasema huku akiipapasa bastola yake!



    “Unataka kufanya nini?” Getruda akamuuliza John aliyekuwa anaanza kutoka.



    “Nitamtwanga risasi! Anatufuata sana mtu huyu… yaani tunamwangalia atuharibie?”



    “Usifanye hivyo John, yule ni polisi, usije ukazua mengine!”



    “Sasa tufanyeje?”



    “Nakwambia utaharibu kila kitu, kama nilivyokwambia huyo ni polisi, halafu umuue hadharani? Si Jeshi zima la Polisi litahamia hapa nyumbani kwako? Hapana!”



    “Oh, nitafanya nini sasa? Shenzi sana!” John Bosho akaendelea kusema huku akijipiga katika paji la uso!



    “Panga mpango mwingine mzuri!”



    “Ok, ngoja nitapanga mpango mwingine kabambe na vijana wangu wa kazi. Tena nitawataarifu usiku wa leo, tukutane katika maskani yetu, Machimbo ya Mawe! Baada ya kukutana huko, tutajua la kufanya!” John Bosho akasema huku akirudi pale sebuleni na kukaa kwenye sofa!



    Ama kweli alikuwa amechanganyikiwa!



    “Hilo ni jambo la maana…” akamaliza kusema Getruda, ambaye naye alikaa kwenye sofa.



    Hakika walikuwa wamechanganyikiwa!



    John Bosho akaona kuwa mipango yake inaendelea kwenda mrama. Na cha zaidi kilichomuumiza, ni juu ya yule mganga wao, Mzee Chiloto Bandua, wa Chamazi, ambaye alimpatia dawa ya kumfanya asiweze kukamatwa, au kujulikana kama ndiye aliyemuua Anita! Mbona sasa imekuwa vile?



    “Vipi John, mbona hivi?” Getruda akamuuliza baada ya kuona akiendelea kuwaza!



    “Aisee…ni lazima niwaze!”



    “Punguza mawazo…”



    “Unajua kuna kitu kimoja kinanitatiza. Ilikuwa ni siri, lakini inabidi nikwambie…”



    “Ni kitu gani hicho? Mbona sikuelewi!”



    “Utanielewa tu,” John Bosho akamwambia na kuongeza. “Ngoja nikuambie ukweli wenyewe muda siyo mrefu!”



    John Bosho na Getruda walikuwa bado wamekaa pale sebuleni, ikiwa ni baada ya Kachero Inspekta Malik kuondoka na kurudi kituoni. Wakati huo, Getruda alikuwa akisubiri kusimuliwa ile siri iliyokuwa inamsumbua John, baada ya kushindwa kwa jaribio la kumuua  kachero Inspekta Malik kwa sumu ya nyongo ya Mamba, iliyotiwa ndani ya juisi.



    “Nisikilize kwa makini Getruda…” John Bosho akamwambia kwa msisitizo.



    “Ndiyo nakusikiliza…” Getruda akasema huku akimwangalia na kumsikiliza kwa makini.



    “Unajua baada ya mimi kumuua mchumba wangu, Anita, ilinibidi nijihami…”



    “Ujihami kivipi?”



    “Ili nisijulikane kama mimi ndiye niliyefanya mauaji hayo, niliamua kwenda kwa mganga mmoja  wa jadi, ambaye huwa anatusaidia katika shughuli zetu. Baada ya kumwendea akanipa masharti, ambayo niliyatekeleza. Lakini nashangaa mambo yamezidi kuwa magumu kiasi cha kuanza kuandamwa! Sasa sijui kama kanitapeli?”



    “Kwani huyo mganga alikupa masharti gani?”



    “Ni kumpelekea baadhi ya viungo vya mwili wa Anita!”



    “Viungo vya mwili wa Anita?”



    “Ndiyo manaake…”



    “Ina maana ni nyie mlifukua kaburi lake usiku?” Getruda akauliza huku amefumba macho!



    “Ndiyo sisi. Ni kama nilivyokueleza kwamba yalikuwa ni masharti magumu niliyopewa na mganga huyo anayejulikana kwa jina, mzee Chiloto. Lakini cha ajabu  ndicho hiki ninachoendelea kuona kuwa ni uongo mtupu! Amechukua fedha yangu bure mzee yule mshenzi!



    “Oh, Mungu wangu!” Getruda akasema!



    “Ndiyo hivyo Getruda. Sasa cha muhimu, mimi nimepanga kwamba nimwendee nyumbani kwake, ili anieleze ukweli wa jambo hili! Kabla mimi sijatiwa mbaroni, lazima na yeye awe kuzimu!” John Bosho akasema kwa msisitizo!



    “Ina maana unataka kuua tena?”



    “Ndiyo…lazima nimmalize!”



    “Mungu wangu!”



    “Hakuna cha kusema Mungu wangu! Jiandae tuondoke wote!”



    “Unasema tuondoke wote?”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Ndiyo! Habaki mtu hapa! Na baada ya kummaliza huyo mganga, ndiyo tunakwenda Machimbo ya Mawe, kukutana na vijana wangu. Ni katika kupanga mpango wa kummaliza Kachero Inspekta Malik!”



    Getruda hakusema kitu chochote zaidi ya kubaki amechanganyikiwa! Alikuwa mbele ya muuaji!



    Hakuwa na la kufanya!



    ********     





    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog