Search This Blog

Thursday 27 October 2022

MUUAJI ASAKWE - 2

 









    Simulizi : Muuaji Asakwe

    Sehemu Ya Pili (2)





    ALIPOMALIZA kuongea kwa simu na rafiki yake, Getruda, Anita alijibwaga tena kwenye sofa. Wakati akiwa bado amekaa hapo, mara mlango wa nje uligongwa mara mbili. Akashtuka na kubaki akiuangalia huo mlango mkubwa kana kwamba ndiyo kwanza alikuwa ameuona! Mapigo ya moyo wake yakapiga kwa kasi, Je, ni nani anayegonga usiku huo? Hakujua!



    Kabla hajanyanyuka kwenda kuufungua huo mlango, mara ukafunguliwa na John Bosho, ambaye aliingia hadi ndani hapo sebuleni, ambapo Anita akiwa bado amekaa, alibaki akimwangalia tu bila kumsemesha, hadi alipoenda kujikalia kwenye sofa dogo la pembeni. Hakutaka kumsemesha Anita ambaye alionekana kuchukia sana, ukizingatia siyo muda mrefu alikuwa akinywa soda yake taratibu tu, kana kwamba hakumwona alivyokuwa akiingia.



    “Anita mpenzi wangu…” John Bosho akaamua kumwita baada ya kuvumilia kunyamaza kwa muda.



    “Bee,” Anita akaitikia huku akimwangalia kwa huzuni.



    “Naona umechukia sana…” John akamwambia kwa sauti ndogo.



    “Ni kweli…nimechukia sana!” Anita akamwambia na kuendelea. “Na hata ninapokuona hapa, ni kwamba naona kichefuchefu!”



    “Unaona kichefuchefu?” John Bosho akamuuliza!



    “Ndiyo, naona kichefichefu! Huwezi kunichanganya mimi na rafiki yangu, Getruda!”



    “Ndiyo maana nimekuja tuyamalize mpenzi wangu…”



    “Uyamalize na nani?”



    “Si wewe mchumba wangu?”



    “Haitawezekana kamwe!” Anita akamwambia na kuendelea. “Yaani kuanzia leo hii mimi na wewe basi! Uchumba wetu uishie hapa hapa! Nakuchukia sana!”



    “Kwa nini iwe hivyo?”



    “Nimejaribu kukuchunguza kwa muda mrefu sasa, na kugundua kuwa wewe siyo mwaminifu kabisa. Hivyo nilichopanga mimi ni kuuvunja uchumba wetu rasmi, hakuna mjadala!”



    “Usifanye hivyo Anita…” John Bosho akawa anambembeleza.



    “Ndivyo nilivyoamua, mwanaume wewe, unaweza kuniua kwa ukimwi!”



    “Usiseme hivyo, ukimwi tena?”



    “Ndiyo, huoni unavyoutembeza? Huridhiki na mimi mchumba wako?” Anita akaendelea kusema na kuendelea. “Na kwa taarifa yako, na hii pete ya uchumba uliyonivisha naivua hii hapa!”



    “Usiivue tafadhali!” John Bosho akaendelea kumsihi.



    “Sikuelewi kabisa!” Anita akasema huku akiivua hiyo pete iliyotengenezwa kwa dhahabu!



    John Bosho akabaki akitumbua macho! Baada ya kumaliza kuivua, akampa  pete hiyo ya uchumba kwa kumpatia mkononi mwake, na Jophn akabaki amechanganyikiwa na kuiangalia, kwani hakuamini hicho alichokuwa anakiona! Yaani kurudishiwa pete yake, ambayo alikuwa ameshamvalisha?



    “Halafu hatua itakayofuata…” Anita akaendelea kumhabarisha. “Ni kuirudisha nyumba hii uliyopangishia kwa mwenyewe, na mimi narudi nyumbani kwa wazazi wangu, kule Kiwalani, ili niweze kukuachia uhuru wa kutanua vizuri na Getruda! Nimeamua hivyo na hakuna wa kuyabadili mawazo yangu!”



    “Unasema unarudi nyumbani kwa wazazi wako?” John Bosho akamuuliza kana kwamba alikuwa hajamsikia vizuri!



    “Sina jinsi John. Ukweli ni kwamba nilikupenda sana,” Anita akamwambia na kuendelea. “Lakini sina budi kufanya hivyo!”



    “Sijakupata vizuri Anita, ina maana na hii nyumba niliyokupangishia?”



    “Hakuna jinsi John, itabidi tuirudishe kwa mwenyewe!”



    “Oh,”  John Bosho akaishia kuguna huku akiendelea kumwangalia mchumba wake huyo alivyokuwa amechukua kupita maelezo.



    “Halafu kitu kingine ambacho nitakifanya John,” Anita akaendelea kumwambia. “Itabidi nitoe siri zako zote, ambazo nilikuwa nimezificha muda mrefu sasa, kuwa wewe ni mtu mwovu, ni jambazi!”



    “Mh! Umefika mbali sasa Anita!” John Bosho akamwambia huku akimwangalia kwa hamaki!



    “hapana, sijafika mbali!”



    “Ina maana unataka kunichoma?” John Bosho akasema huku akiyatoa macho yake pima!



    “Ndiyo, nitafanya hivyo! Na kuanzia sasa hivi ondoka hapa nyumbani!” Anita akamwambia huku akiwa  amechachamaa na povu likimtoka mdomoni!



    “Yaani unanifukuza Anita? Hakika siamini!”



    “Ndiyo, kuanzia sasa amini! Sitaki mawasiliano na wewe!”



    “Hutaki mawasiliano na mimi sivyo?”



    “Ndiyo, sitaki!”



    “Basi, na mimi nakushauri kuwa fikiria mara mbili mbili juu ya kauli yako ya kutaka kunichoma kwa Jeshi la Polisi! Achana na wazo hilo kabisa!” John Bosho akamwambia Getruda huku akinyanyuka!



    “Kwani utafanya nini?”



    “Nitajua cha kufanya, naona unajiamini sana wakati unatambua fika kuwa mimi ni mtu wa aina gani!”



    “Kabla hujanidhuru, utakuwa umeshatiwa mbaroni!”



    “Haya, tuone nani mtoto wa mjini! Mimi naondoka zangu!” John Bosho akamwambia Anita!



    Baada ya mabishano yale, John Bosho akaamua kuondoka, kwani hakutaka kubishana na Anita, kitu ambacho kingejaza watu usiku ule. Lakini baada ya kuondoka, alibaki akiwa amechanganyikiwa baada ya Anita kumwambia kuwa angemchoma kwa Jeshi la Polisi, kuwa anajihusisha na ujambazi!



    Jambo hilo ndilo lililomuuma zaidi John Bosho! Aliona kama Anita angetoa siri zake, basi huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kuangamia kwake! Hivyo akaamua jambo moja tu, ni kumwondoa uhai wake haraka iwezekanavyo!



    *********         



    WIKI moja ilipita tokea John Bosho na Anita kutibuana, mara baada ya kugundulika kuwa yeye ana uhusiano wa kimapenzi na Getruda, rafiki yake Anita. Ukweli ni kwamba wiki hiyo ilikuwa ngumu sana kwa wapenzi wale waliokuwa wameshazoeana. Kila mmoja hakuamini kile kilichokuwa kimetokea zaidi ya kuuamia rohoni.



    John Bosho aliendela kumwomba msamaha na kumbembeleza sana, mchumba wake, Anita, lakini hakuambulia kitu zaidi ya kupewa maneno ya kashfa. Kwa vile alikuwa bado anampenda, roho ilikuwa inamuuma sana, hivyo akaamua kukutana na vijana wake wa kazi ili kupanga mkakati maalum.



    Walikuwa ni vijana waliokuwa wanajulikana kwa majina ya, Chogolo, Muba, Kessy na Chikwala, ili awaelezee juu ya azma yake ya kutaka kumwondoa uhai Anita, aliyetishia kuitoa siri zake. Kwa kumsikiliza bosi wao, vijana hao wakakubaliana naye na kuzidi kumpa moyo! Ni kumtoa uhai wake mara moja!



    Sasa kilichobaki kwa John Bosho, ilikuwa ni juu ya kupanga kifo cha Anita kitakavyotekelezwa kwa ufanisi wa hali ya juu. Kwa upande wake hakupenda kutumia silaha yake katika kutimiza lengo lake, isipokuwa aliamua kutumia sumu kali aina ya nyongo ya Mamba, ambayo huua mara moja mara baada ya mlengwa kuitumia.



    Sumu hiyo kali, John Bosho alikuwa anaihifadhi nyumbani kwake kwa malengo maalum, ikiwa katika hali ya unga, lakini akitaka kuitumia, huichanganya na maji tayari kwa kudunga sindano, au unga huo  kwa kuunyunyizia sehemu husika anayokusudia, kama vile kwenye vyakula, maji ya kunywa, vinywaji nk. Hivyo, John Bosho aliamua kummaliza Anita kwa kumdunga sindano ya sumu ile itakayotiwa ndani ya bomba la sindano.



    Basi siku hiyo ya kutekeleza kazi yake, John aliiandaa sumu hiyo na kuichanganya na maji, halafu akaiweka kwenye kichupa kidogo, ambacho alikihifadhi ndani ya droo ya gari lake. Baada ya kukamilisha kila kitu, akatoka nje ya nyumba yake, eneo hilo la Ukonga, halafu akapanda gari lake aina ya Toyota Harrier, kuelekea kwenye mizunguko yake mingine ya kibiashara katikati ya jiji la Dare s Salaam.



    Alipomaliza mizunguko yake hiyo, ndipo aliposhika uelekea wa kwenda eneo hilo la Tabata Mawenzi, alipokuwa anaishi Anita, mchumba wake waliohitilafiana. Wakati huo ilikuwa imetimu saa saba na nusu za mchana, na yeye alijua kwamba  Anita alikuwepo nyumbani. Hivyo aliifiata Barabara ya Mandela moja kwa moja kutokea Biguruni. Na alipfika eneo la Tabata, alipinda kulia na kuifuata barabara inayoelekea maeneo ya Tabata Bima na kwingineko.



    Aliifuata barabara hiyo kwa mwendo wa taratibu tu na baada ya kufika eneo la Tabata Aroma, John Bosho alilisimamisha gari kando ya barabara karibu na kituo cha daladala, halafu akashuka garini na kuelekea kwenye duka moja la kuuza dawa za binadamu, lililokuwa katika jengo lile Aroma, lenye ghorofa tatu.



    John Bosho akaingia ndani ya duka hilo kwa kuusukuma mlango wa kioo uliokuwa na fremu ya aluminiam, na baada ya kuingia ndani, alipokewa na hewa ya ubaridi wa kiyoyozi. Humo ndani  alimkuta mwanadada mmoja mwenye umri wakati, aliyekuwa anauza dawa, ambaye alimkaribisha kwa sauti ya kibiashara:



    “Karibu…”



    “Ahsante…” John Bosho akasema huku akimkagua!
    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Nikusaidie…” mwanadada yule akamwambia.



    “Ninahitaji bomba la sindano?”  John akamwambia.



    “Unahitaji mangapi?…” mwanadada yule akamuuliza.



    “Nahitaji bomba moja la sindano…”



    “Bomba moja tu?” Muuzaji akauliza baada ya kumshangaa kwa kuchukua bomba moja tu, kwani alitakiwa achukue zaidi ya moja.



    “Ndiyo, moja linatosha, kwani vipi?”tu…” John akamwambia huku akimwangalia mara mbili mbili!



     “Naona ungechukua na akiba…moja halitoshi…”



    “Kwani unajua nataka kufanyia kazi gani?”



    “Si kwa kuchomea dawa?”



    “Basi moja linatosha…”



    “Haya…” muuzaji huyo akamwambia.



    Muuzaji wa dawa akafungua kabati lililokuwa linatunzia dawa, halafu akachukua lile bomba la sidano na kumwekea kwenye bahasha ya rangi nyeupe kwa ajili ya kuwapa wateja. John Bosho akalipokea na kumlipa fedha baada ya kuchomoa noti ya shilingi efu kumi kwenye pochi yake, na kabla hajarudishiwa chenji yake, akaanza kuondoka kuonyesha alikuwa na haraka sana!



    John Bosho alifanya hivyo, kwani hakutaka kuulizwa maswali mengi na yule muuzaji, na pia aliogopa sije akamkariri sura itakapogundulika kama ni yeye atakayekuwa ametekeleza mauaji ya Anita, ambapo ndipo alipokuwa anaelekea huko!



    “Kaka chenji yako!” Muuzaji yule akamwambia baada ya kuona amesahau!



    “Ah, hiyo chenji chukua tu,” John akamwambia, halafu akatoka nje kwa hatua za haraka.



    “Ahsante,” muuzaji akasema huku akishangaa kuachiwa fedha na mteja yule!



    John Bosho alipofika nje sehemu ile alikopaki gari lake, akaufungua mlango na kuingia ndani. Kabla ya kuondoa gari, akakaa kwa muda, ambapo alifungua droo moja iliyokuwa hapo mbele kwenye ndashibodi ya gari, halafu akatoa kichupa kidogo, ambacho  kilichokuwa na ule mchanganyiko wa maji na sumu kali ya nyongo ya Mamba. Akakakiangalia kichupa hicho huku akitabasamu, hasa akifikiria kuwa ndiyo alikuwa anakwenda kuitumia kwa mlengwa aliyemkusudia!



    Mara baada ya kukiangalia kile kichupa kwa muda, akalitoa lile bomba la sindano ndani ya bahasha, na kuinyonya ile sumu kiasi cha kulijaza lile bomba lote, kisha akalirudisha ndani ya bahasha tena na kichupa kukirudisha ndani ya droo. Hapo ndipo alipovuta pumzi ya nguvu na kuishusha, halafu akayatupa macho yake pande zote, kulia na kushoto. Hakuna mtu yeyote kati ya wapiti njia aliyemuoa zaidi ya kila mmoja akiwa katika shughuli zake.



    Baada ya kumaliza kuhakikisha hakuna mtu aliyemwona, ndipo John Bosho alipolitia moto gari lake na kuliondoa kwa mwendo wa taratibu, kuliingiza katika barabara kuu, kuelekea Tabata Mawenzi, nyumbani kwa Anita kutimiza azma yake ya kuuondoa uhai wake! Akiwa ndani ya gari huku akiendesha kwa mwendo wa wastani, alichomoa simu yake ya mkononi na kumpigia Anita kumtaarifu kuwa anakwenda hapo nyumbani kwake.



    Simu ikaanza kuita!



    ********        



    MAJIRA ya saa nane za mchana, Anita alikuwepo nyumbani kwake, Tabata Mawenzi. Wakati huo ndiyo alikuwa amepumzika kwenye sofa sebuleni, huku akiwa na mawazo mengi sana. Tokea akorofishane na mchumba wake, John Bosho, alikuwa hana raha kabisa, na alikuwa anapanga kurudisha nyumba na kuondoka haraka sana!



    Simu ya mkononi iliyokuwa juu ya meza ndogo ya kahawa hapo sebuleni, umbali mfupi tu na aliokuwa amekaa kwenye sofa, ilianza kuita. Akanyanyuka kivivu na kuichukua, akiwa na hamu ya kutaka kujua mpigaji wa simu hiyo, hasa ukizingatia siku ile hakuwa katika hali nzuri kabisa, alihitaji kupumzika.



    Lakini Anita alipoangalia namba za mpigaji wa simu hiyo, aliona ni ya siri isiyoonyesha namba ya mpigaji kwa tarakimu, akaduwaa kwanza, halafu akaipokea kwa sauti ndogo, “Anita anaongea…”



    “Oh. hujambo mpenzi wangu?” Upande wa pili wa simu ukasema kwa sauti nzito, ambayo siyo ya mtu mwingine zaidi ya John Bosho, mchumba wake waliokorofishana. Na wakati huo ndiyo alikuwa ndani ya gari lake, akielekea nyumbani kwa Ania katika kutekeleza adhabu yake aliyokuwa amempangia!



    “Si…sijambo…” Anita akaitikia kwa kusita kidogo mara baada ya kuitambua sauti ya huyo mpigaji wa simu hiyo!



    “Ni mimi mchumba wako, John Bosho…” John Bosho akajitambulisha kwani alijua kuwa namba haikusomeka kwenye kioo cha simu.



    “Nimeshajua ni wewe John…unasemaje?” Anita akauliza kwa hasira!



     “Vipi tena?” John Bosho akauliza. “Mbona unakuwa mkali mpenzi Anita?”



    “Mimi siyo mpenzi wako, John …naomba unisahau na usinijue!”



    “Usifanye hivyo…naomba tukutane ili tuweze kulitatua tatizo hili…”  John Bosho akaendelea kumsihi Anita.



    “Haiwezekani, sitaki kuonana na wewe kabisa!” Anita akamwambia na kukata ile simu, huku akifyonza kwa nguvu!



    Baada ya kuikata ile simu, Anita akaiweka mezani na kuendelea kuwaza. Hata hivyo ile simu ikaita tena, mpigaji akiwa ni mtu yule yule mchumba wake, John Bosho! Hivyo akaamua kumsikiliza ingawa ilikuwa kero kwa upande wake!http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Unasemaje? Mimi naona kama unanisumbua!”



    “Naomba uwe mtulivu Anita. Daima mvumilivu hula mbivu…” John akaendelea kumwambia Anita.



    “Sikiliza John. Natumaini wewe ni mtu mwelewa sana! Siwezi kuwa mtulivu…si unajua kwamba umeamua kunisaliti kwa penzi la rafiki yangu Getruda? Basi endelea naye na mimi uniache nilivyo!” Anita akamwambia kwa sauti iliyojaa uchungu mwingi!



    “Ok, hayo tuyaache…mimi nitakutembelea hapo nyumbani jioni ya leo ili tuyamalize. Mbona ni mambo madogo sana?”



    “Wewe unaona haya ni mambo madogo? Hapana, naomba usije John…” Anita akaendelea kumwambia!



    “Sasa nisikilize kwa makini sana Anita,” John Bosho akamwambia na kuendelea. “Mimi nitakuja hapo nyumbani upende usipende. Hakuna mtu asiyejua kuwa mimi ni mmoja wa wahusika wa hapo. Nafikiri unanijua kwamba mimi ni mtu wa aina gani! Ukicheza nakuondoa uhai wako mara moja!”



    “Oh, Mungu wangu!”



    “Mwombe sana huyo Mungu wako!” John akamaliza kusema!



    Simu ikakatwa!



    Anita akavuta pumzi ndefu na kuzishusha, halafu akajiegemeza kwenye sofa huku mawazo yake yakiwa mbali. Hakujua John Bosho alikuwa anahitaji kitu gani kutoka kwake, wakati alishamwambia kuwa hataki uchumba tena, na pete yake alikuwa ameshamvulia na kumrudishia!



    Anita aliiangalia saa yake, ambayo ilionyesha imetimu saa nane mchana, hivyo hakuwa na jingine zaidi ya kuingia chumbani ili kupumzika chakula kiteremke. Baada ya kujilaza tu, alipitiwa na usingizi mzito uliochanganyika na mawazo aliyokuwa anawaza, na pia jinsi John alivyomchanganya!



    Anita alianza kuota ndoto za kutisha, huku akikumbwa na majinamizi, ikiwa ni ndoto ambayo alikuwa hajawahi kuota hata siku moja, ikiashiria ni ndoto ya kifo! Ndani ya usingizi huo, aliota akijiona anaruka angani kwa kasi, akiyapita mabonde na milima mikubwa, ambayo aliweza kuiona kwa chini. Hatimaye akaenda kutua juu ya mlima mmoja mrefu uliotengenishwa na bonde lenye kina kirefu ajabu.



    Kwa mbele nako aliuona mlima mwingine mrefu kama ule aliokuwa amesimama yeye, ambao uliwatengenisha kwa lile bonde. Mara muungurumo kama wa radi ulitokea na kulipuka katika mlima ule wa pili, ambapo alitokea mtu mmoja aliyekuwa amevalia mavazi meupe yanayong’aa. Mtu yule akanyoosha mkono wake wa kulia na kusema kwa sauti iliyokuwa inatoka kwa mwangwi uliotetemesha!



    “Anitaaa….aaaa!”



    “Beeee!” Anita akaitikia kwa hofu!



    “Wewe mwanadamu…nakukaribisha huku kwetu!” Mtu yule akaendelea kumwambia!



    “Hivi huku ni wapi?” Anita akauliza huku akiwa na wasiwasi mkubwa.



    “Nilisikilize kwa makini wewe mwanadamu. Huku ni peponi!”



    “Lakini mimi siwezi kufika huko mpaka nivuke bonde hili!”



    “Ni kweli huwezi kuvuka katika bonde hili!” Mtu huyo akamwambia na kuongeza. “Unahitaji kutubu dhambi zako…na ukitubu tutakukaribisha!”



    “Oh, basi nitatubu ili  niweze kuvuka…”



    “Nasikitika sana mwanadamu! Umechelewa…huu siyo muda wake!”



    “Oh, Mungu wangu! Kwa nini?”



    “Napenda kukutaarifu ujiandae…Muda siyo mrefu utakuja huku. Lakini hutanifikia katika himaya hii ya peponi.!”



    “Sitafanikiwa?” Anita akauliza. “Isipokuwa?”



    “Ni lazima utazama ndani ya bonde hili!”



    “Kwa nini nizame?”



    “Utazama kwa ajili ya dhambi zako zilizotukuka!”



    “Mamaaa..aaa!” Anita akalia kwa kupiga ukulele mkubwa! Ni ukulele ambao ulitoa mwangwi ulioenea kote!



    “Haya, jiandae kuja huku! Karibu sana katika himaya ya peponi” Mtu huyo akamwambia huku akimnyooshea kidole!



    Muungurumo mkubwa ukatokea! Mtu huyo akazama katika mawingu meupe yaliyokuwa yametanda angani!



    “Ooohps!” Anita akapiga yowe kubwa na kushtuka katika usingizi ule wa mchana!



    Anita akayafikicha macho yake na kuona kuwa alikuwa ndani ya chumba chake, ambapo alikuwa amelala siyo muda mrefu. Hatimaye baada ya kugundua kuwa alikuwa chumbani mwake, akashuka kitandani na kukaa huku akitafakari ndoto ile. Ukweli ni mkwamba ilikuwa inatisha ilikuwa inatisha!



    Je, iliashiria kitu gani?



    Hivyo basi, Anita akanyanyuka kutoka pale  kitandani. Halafu akachukua taulo lililokuwa limetundikwa, pamoja na upande wa kitenge, ambao alijifunga na kuamua kwenda kujimwagia maji ndani ya bafu lililokuwa mle ndani, ili kuondoa uchovu uliotokana na usingizi wa mchana.



            ********  



    John Bosho alisimamisha gari lake katika uwanja mdogo uliokuwa mbele ya maegesho ya kuegesha magari, jirani na Mawenzi Bar, eneo la Tabata Mawenzi. Sehemu hiyo iliyokuwa na miti ya muarobaini iliyokuwa na kivuli, pia, palikuwa na magari mengine kama matatu hivi yaliyokuwa yamepaki hapo, hivyo yeye akalipaki la kwake katikati ya hayo magari.



    Majira hayo ya saa tisa za alasiri, jua lilikuwa bado ni kali, kiasi cha kuleta kero kwa watembea kwa miguu na wasafiri wanaotumia mabasi ya daladala, ambao wengine walijificha katika vivuli vya miti. Baada ya kupaki lile gari, John akashuka na kuufunga mlango wa gari huku akihakikisha kama ameufunga vizuri, halafu akaondoka kwa mwendo wa taratibu kuufuata uchochoro mmoja uliotenganisha nyumba na nyumba.



    John Bosho alitembea kwa mwendo wa kawaida tu, huku katika mkononiwake wa kushoto ameshika bahasha ndogo iliyokuwa na kitu muhimu, bomba moja la sindano lililokuwa na sumu kali ndani yake, ambayo ni ya kumshughulikia mchumba wake, Anita. Hivyo akaendelea kuufuata ule uchochoro na kutokea kwenye eneo hilo lililokuwa liimezungukwa na uzio wa ukuta uliojengwa kwa matofali. Ndani yake ndipo palipokuwa na nyumba kama tano hivi, ambapo nyumba aliyopanga Anita ilikuwa moja wapo.



    Pale John akasimama kwa muda huku akichungulia ndani kwa kutumia matundu madogo yaliyokuwa katika ukuta, ambayo yalitengenezwa kama urembo, na pia kuwezesha upepo kuingia ndani, lakini hakuona mtu yeyote, aliyekuwa pale uani. Palikuwa kimya kabisa, na kitu alichoweza kuona, ni bustani ya maua na miti iliyokuwa pale.



    Basi, ndani ya nyumba moja wapo, ambayo haikuwa mbali na uzio wa ukuta, ambapo pia siyo mbali na hapo alipokuwa amesimama nje ya ukuta,  ndipo alipokuwa anaishi Anita, mchumba wake. Vilevile, wakati huo alikuwepo ndani kwake, ikiwa ni muda mfupi tu tokea amempigia simu na kumjulisha kuwa yeye atakuwa mgeni wake, ingawa alikataa.



    Hapo alipokuwa amesimama John Bosho, palikuwa na miti ya muarobaini iliyofungamana. Hivyo hakupoteza muda, akauruka ule uzio kiufundi bila kuonekana na mtu yeyote hadi alipoibukia ndani ya ua wa nyumba hiyo, umbali mfupi kutoka katika nyumba anayoishi Anita. Baada ya kuingia, akajibanza kwenye kona moja iliyokuwa na maua yaliyofungamana, tayari kulivizia windo lake, mchumba wake, Anita!



    Ni kwamba John Bosho alikuwa amepanga aingie mle ndani ya nyumba ya Anita bila kuonekana na mtu yeyote, ili amfungie kazi, ukizingatia alifika pale kwa kazi moja tu ya kuua, na si vinginevyo! Hivyo akaendelea kubanisha pale kwenye kivuli cha maua ili kuvuta subira mpaka atakapomwingilia mle ndani kwake kwa kupitia katika mlango mkubwa aliokuwa anauangalia kwa makini!



    Baada ya kuhakikisha kila kitu kilikuwa shwari pale uani, John Bosho alijitoa pale mafichoni na kuuendea mlango ule wa kuingia ndani ya nyumba ya Anita. Baada ya kuufika, akaufungua taratibu na kuingia ndani huku akinyata. Akaanza kumtafuta Anita kila kona, hadi alipogundua kuwa alikuwa ameingia bafuni kuoga na kuufunga mlango bila komeo, kwa vile ilikuwa ni ndani kwake, na alikuwa peke yake.



    John Bosho aliuendea mlango ule wa bafuni, ambao pia aliufungua taratibu, ambapo pia aliweza kumwona Anita akiuvua ule upande wa kitenge aliokuwa amejifunga pamoja na taulo, na vyote kuvitundika kwenye kamba iliyokuwa mle ndani. Akabaki uchi na kujiandaa kujimwagia maji bila kujua kuwa kuna mtu aliyekuwa anamwinda pale mlangoni!



            ********



    MARA baada ya Anita kuvua kienge na kubakia uchi kama alivyozaliwa, na kabla hajajimwagia maji, alijiangalia takriban dakika moja hivi, na kujiona alivyokuwa na umbile zuri na la kuoendeza. Hapohapo akajiuliza, imekuwaje John Bosho, mchumba wake, amkinai na kumkimbilia Getruda rafiki yake? Ni kitu gani alichokosa mwilini mwake?



    Hata hivyo, Anita akayatupilia mbali mawazo hayo, halafu akaliangalia bomba la mvua lililokuwa juu, ambalo alikuwa tayari kulifungua ili aanze kujimwagia maji. Lakini kabla hajafanya lolote, akashtukia akirukiwa na kiumbe chenye nguvu mithili ya mnyama,  Simba, na kiumbe hicho kikamng’ang’ania maungoni mwake!



    Anita alichanganyikiwa kwa kitendo hicho kilichotokea ghafla kana kwamba alikuwa ndotoni, na kutaka kupiga kelele za kuomba msaada. Hata hivyo sauti yake haikuweza kutoka, kwani alizibwa mdomo na mkono wenye nguvu nyingi!



    “Oooohpsi!” Anita akapiga kelele ambayo haikuweza kusikika mbali kwa vile alikuwa amezibwa mdomo!



    “Tulia!” John Bosho akamwambia kwa sauti ndogo lakini nzito!



    “Ooh! Unataka nini?” Anita akamuuliza!



    “Ni mimi John Bosho!” Akamwambia kwa sauti kavu na kuendelea “Nimekuja kama nilivyokwambia muda siyo mrefu kwenye simu! Hivyo nakusihi utulie kimya kabla sijakumaliza!”



    “Oohps….Ooohps!” Anita akatoa sauti baada ya mdomo wake kuachiwa na John aliyekuwa amemziba kwa mkono wenye misuli!



    “Nakuonya tena! Tulia!” John Bosho akaendelea kumwambia huku akimwonyesha bastola aliyokuwa ameikamata mkononi!



    “Oh, umepitia wapi mwanaume wewe?” Anita akamuuliza huku bado wasiwasi mwingi umemjaa!



    “Unashangaa? Nimepitia mlangoni!” John Bosho akaendelea kusema huku amekunja uso wake! Ni uso uliokuwa unatisha mithili ya jitu la porini!



    “Mbona unanifuata sana?” Anita akamuuliza huku akiwa na wasiwasi!



    “Ni kama nilivyokwambia mwanzo Anita!..” John Bosho akamwambia huku akimwangalia kwa uchu wa ngono, ukizingatia alikuwa na umbile zuri la kike lenye kutamanisha! Halafu akamvutia kwake na kutaka kumkumbatia!



    “Tafadhali toka, usiniguse!” Anita akamwambia huku akikunja uso wake!



    “Lazima nikuguse mpenzi!”



    “Nitakupigia kelele!” Anita akasema huku akimsukuma John Bosho.



    “Huwezi kupiga kelele, naomba uwe mtulivu, na kutulia kwako ndiyo usalama wa maisha yako!” John akamwambia Anita huku akimfuata!



    “Unataka kufanya nini?”



    “Nataka nikufanye kwanza, halafu adhabu nyingine ifuate baadaye!”



    “Ooohpsi!” Anita akapiga ukelele mdogo!



    “Usiniwangie mchana!” John Bosho akamwambia Anita. Halafu akamkamata kwa nguvu na kumwangusha chini sakafuni!



    Kwa vile Anita alikuwa uchi wa mnyama, uchu wa ngono ukaendelea kumwandama John Bosho, na baada ya kumwangusha chini, akafungua zipu ya suruali yake na kutoa ‘dhakari’ yake. Akaanza kumbaka  Anita mbaye kwa muda ule hakuwa na nguvu yoyote baada ya John kumbana kwa nguvu pale sakafuni hadi alipomaliza haja yake huku akichekelea!



    Ni unyama wa kutisha!



    Alipomaliza kumbaka Anita, John Bosho akampiga kofi moja la nguvu lililomfanya achanganyikiwe na kuona nyota nyota! Halafu bila kupoteza, akachukua ile bahasha ndogo aliyokuwa nayo, na ndani yake kulikuwa na bomba la sindano, lililokuwa na sumu kali aliyokuwa ameitayarisha kwa ajili ya kazi ile. Akamchoma Anita na sumu yote ikamwingia mwilini mwake!



    Baada ya John kumaliza kumchoma ile sindano, akalichomoa lile bomba na kulitia ndani ya ile bahasha, ambayo aliiacha kando ya mwili wa Anita uliokuwa umelala pale kwenye sakafu ya bafuni. John akasimama kwa muda huku akiuangalia ule mwili mwororo wa Anita, ambao muda siyo mrefu alikuwa akijiburudisha juu yake. Akatikisa kichwa kwa uamuzi ule alioamua kumfanyia mwanadada huyo, ambaye kamwe hakupaswa kupewa adhabu kama ile ya kinyama!



    Kwa upande wa John, aliamua kumuua Anita kwa kutumia njia ya sumu, kwani hakupenda kutumia bastola ingawa alikuwa nayo muda wote. Sumu ile ikaendelea kuingia na kusambaa katika mwili wa Anita na kumfanya apate maumivu makali sana huku nguvu zikimwishia na kuona giza!



    “Ooohpss!” Anita akendelea kupiga kelele!



    “Utakoma kuringa!” John Bosho akaendelea kumsimanga!



    “Oh, unaniua John…oh!”                        



    “Sikuwa na jinsi…siri zangu nyingi unazijua! Hivyo huna budi kufa!”



    “Oh, Mungu wangu!” Anita akaendelea kusema huku akifumba macho!



    “Kwa heri Anita…kawasalimie kuzimu!” John Bosho akamwambia huku akijiandaa kuondoka.



    “Mungu atalipa…” Anita akamaliza kusema huku roho ikianza kuachana na mwili!



    Baada ya kuhakikisha Anita amekufa, John Bosho akatoka  mle ndani ya bafu lile kwa njia ileile aliyoingia nayo, hadi alipofika nje. Halafu akatoka nje kabisa wa nyumba ile, kwa kuuruka ukuta ule wa upande wa nyuma na kutokomea kuufuata ule uchochoro hadi sehemu ile aliyokuwa amepaki gari lake. Hakuna mtu yeyote aliyemshtukia kuhusiana na mauaji yale aliyofanya, na alipolifikia gari lake akapanda na kuondoka eneo lile haraka sana akiwa na matumaini!



    Baada ya kufika mbali na eneo lile la tukio, akiwa ndani ya gari lake, ndipo John Bosho alimpigia simu Getruda, na kumjulisha kuwa alishamaliza kazi ya kumuua mchumba wake, Anita!



    “Haloo…John…” Getruda akasema.



    “Ndiyo Getu…” John Bosho naye akasema.



    “Unasemaje?”



    “Nakujulisha kwa mimi ndiyo nimetoka kummaliza Anita!”



    “Umemuua?”



    “Ndiyo!”



    “Oh, Mungu wangu!”



    “Ni kama nilivyokuwa nimepanga! Sasa nakuonya kwamba usije ukatoa siri hiyo! Hakuna aliyeona!”



    “Oh, siwezi kusema…”



    “Haya kwaheri!” John Bosho akasema na kukata simu!



    Upande wa pili alipokuwa Getruda, alibaki ameing’ang’ania simu yake mkononi! Alikuwa amechanganyikiwa sana, yaani amemuua mchumba wake Anita?



    Hakuamini!



    *******



    KELELE za kuomba msaada ndizo zilizowashtua majirani waliokuwa wanaishi katika nyumba nne zilizokuwa mle ndani ya uzio alipokuwa anaishi Anita, ambao walikuwa vyumbani mwao, pamoja na majirani wengine wanaozizunguka nyumba hizo zilizojengwa kwa mtindo wa kupendeza ndani ya uzio madhubuti.



    Ni kelele ambazo Anita alipiga pale mwanzoni wakati John Bosho alipokuwa akimdhibiti kule ndani kwake, bafuni, katika kutaka kumtoa roho yake. Hakika ni kelele zilisikika kama mtu aliyekuwa anakoroma kwa kubanwa pumzi. Majirani walitoka vyumbani mwao haraka haraka, ndani ya zile nyumba nyingine ziliyokuwa jirani na anayoishi.



    Majirani hao walikuwa pamoja na mama mwenye nyumba aliyopanga Anita, Bi. Debora Mjema, ambaye naye alikuwa anaishi humohumo katika moja ya nyumba hizo tano. Halafu wakaelekea ndani ya nyumba hiyo aliyopanga, iliyokuwa hatua chache, ambapo kelele zile zilitokea. Baada ya kufika pale nje, walikuta ule mlango mkubwa umefungwa kwa ndani bila komeo.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Haraka wakaufungua mlango ili kujua kilichokuwa kimemsibu mwanadada Anita, na kumfanya apige makelele ya kuomba msaada. Hatimaye majirani wawili walifanikiwa kuingia mle ndani ya bafu alilokuwa anaoga. Wote walikuwa ni wa wanaume, ambao baada ya kuingia walishangaa kuukuta mwili wa Anita ukiwa umelala sakafuni umetulia kimya, tena ukiwa uchi wa mnyama!



    Mwili huo wa Anita uliokuwa bado umelala pale sakafuni, ulionyesha dalili zote kwamba alikuwa ameshakata roho muda mrefu! Michirizi ya damu ilionekana ikichuruzika kutoka mdomoni na puani, kiasi cha kuwafanya wale wanaume wawili watoke nje mbio, hadi walipofika sebuleni!



    “Kuna nini jamani?” Mtu mmoja akauliza kati ya wale majirani.



    “Mh, hatari!” Akajibu mmoja wa watu wawili waliotoka mle bafuni kuangalia!



    “Hatari ya nini?”



    “Tumemkuta Anita amelala sakafuni,” mtu mwingine akasema na kuongeza. “Tena yuko uchi!”



    “Amefanya nini sasa?” Akaendelea kuuliza kijana mwingine aliyetaka kujua kilichojiri.



    “Bila shaka amepata matatizo mazito!” Mwanaume huyo aliyetoka mle bafuni akasema.



    “Jamani, akina mama ingieni mumvishe hata upande wa khanga!”



    “Ooohpsi!” Akina mama wakapiga kelele baada ya kujua kuwa mambo yalikuwa yameshaharibika!



    Mara baada ya kusema vile, akina mama wawili waliokuwa pale waliingia mle ndani ya bafu. Baada ya kuingia humo bafuni, waliukua mwili wa Anita ukiwa umelala uchi pale sakafuni. Haraka wakatoa upande a kitenge na kuufunika vizuri mwili huo, na hatimaye wakatoka mle bafuni na kujiunga na watu wengine, akiwemo mama mwenye nyumba, ambao walikaa na kutafakari cha kufanya.



    Kwa vile mwili huo wa Anita haukuonyesha uhai wowote,  ndipo ilipojulikana kwamba alikuwa ameshakufa! Watu wengi walianza kukusanyika wakiwemo majirani na wapita njia waliofika kushuhudia tukio lile la kutisha jioni hiyo, kila mmoja akitokwa na machozi ya uchungu kwa kushindwa kuvumilia!



    Vilionekana vikundi kadhaa vya watu waliokuwa wakiongea hili na lile. Hata hivyo hawakujua ni mtu gani aliyesababisha kifo hicho cha kutatanisha! Simu ya dharura ikapigwa na mmoja wa mashuhuda, ili kuwajulisha Jeshi la Polisi juu ya tukio hilo la kifo cha mwanadada, Anita Anthony.



    *********  



    NDANI ya Kituo cha Polisi Buguruni, Jijini Dar es Salaam, shughuli za kazi zilikuwa zinaendelea kama kawaida jioni hiyo. Hata hivyo, baada ya muda, simu ya matukio ya dharura ilipigwa na kupokelewa na askari polisi aliyekuwa zamu katika chumba maalum cha simu, ndani ya Ofisi  ya Idara ya Upelelezi.



    Baada ya kupokelewa kwa simu hiyo iliyoelezea juu ya mauaji yaliyotokea eneo la Tabata Mawenzi jioni hiyo, kwa kuuawa kwa mwanamke ndani ya bafu, ilifanyiwa kazi haraka iwezekanavyo, kwa kujulisha katika sehemu zote zinahusika kwa kutumia redio za mawasiliano.



    Mkuu wa zamu katika Kitengo cha Matukio siku hiyo, alikuwa ni Kachero Inspekta Malik Mkoba, ambaye alikuwepo ofisini muda huo wa saa kumi za jioni. Alikuwa na kazi ya kuyapitia mafaili kadhaa yaliyokuwa mezani mwake, hivyo akajulishwa taarifa hizo za kifo cha mwanadada, Anita, hivyo akaamua kuzifanyia kazi haraka iwezekanavyo, kama ilivyo kawaida katika kazi yake ya upelelezi.



    Kachero Inspekta Malik Mkoba naye aliwasiliana na Mkuu wa Upelelezi wa Kituo cha Polisi Buguruni, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, Alfred Gonzo, ambapo alimpatia taarifa hiyo, na mkuu huyo akampangia kuianza kazi hiyo mara moja, ili kujua chanzo cha mauaji hayo. Ndipo alipotoka ofisini kwake, halafu akateua askari polisi wa Kikosi Maalum waliokuwa zamu.



    Vilevile walikuwepo na wale wa Forensic Bureau Investigation, wakiwemo wataalam, wapiga picha kutoka Kitengo cha Matukio (Scene of  Crime), wakiwemo pia wataalamu wa alama za vidole na wengineo. Baada ya kuwa tayari, askari wote wakatoka na kupanda gari lao aina ya Toyota Land Cruiser, na kuelekea eneo la Tabata, Mawezi, yalipotokea mauaji yale ya aina yake.



    Walikuwa ni askari polisi kumi na mbili, waliokuwa wanaongozwa na Kachero Inspekta Malik Mkoba, ambapo baada ya kufika eneo hilo la tukio,  gari lilisimamishwa nje ya nyumba hiyo, askari wakashuka na kuingia hadi sehemu ya uani, ndani ya nyumba aliyokuwa anaishi Anita. Baada ya kuingia ndani, wakaliendea bafu lile lililokuwa mle ndani, ambapo mwili huo ulikuwepo, umefunikwa shuka ili kuusitiri.



    Kachero Inspekta Malik Mkoba na askari wawili waliingia mle bafuni na kuanza kuuchunguza kwa makini ule mwili. Wakaona kuwa haukuwa na jeraha lolote, ingawa ulianza kuvimba na kuwa na rangi nyeusi. Upande wa kushoto mwa mwili ule, palikuwa na bomba la sindano ya kudungia binadamu, likiwa nusu limezama ndani ya bahasha ndogo ya rangi nyeupe, iliyokuwa  imepigwa muhuri uliokuwa na maandishi yaliyosomeka ‘Kishada Medics.’



    Kachero Inspekta Malik alipomaliza kuisoma ile bahasha, akaitumbukiza ile sindano pamoja na bomba lake, ambavyo vyote alivichunguza kwa muda. Kazi nyingine iliyobakia ilikuwa ni kuwaacha wataalamu wengine, kama mpiga picha, mchukua alama za vidole na mchora ramani kufanya kazi yao. Hakika kila mmoja alifanya kazi yake kwa utaalamu wa hali ya juu ili wasiweze kuharibu ushahidi.



    Kachero Inspekta Malik Mkoba alipomaliza kufanya uchunguzi wake, akaandika baadhi ya mambo muhimu kwenye kitabu chake cha kumbukumbu. Alipomaliza kuandika, akawaamuru wale askari polisi alioongozana nao, waupakie ule mwili wa Anita ndani ya gari, na bila kupoteza muda wakaupakiza kwa kutumia machela, tayari kwa kuupeleka katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa uchunguzi zaidi.



    ********



    UMATI wa watu ulikuwa umejazana katika mtaa mdogo uliokuwa unaelekea katika eneo uzio wa nyumba aliyokuwa anaishi Anita. Jioni hiyo kunako majira ya saa kumi na moja kasorobo, watu hao walikuwa wameshuhudia mwili huo uliofunikwa  vitenge ukiondolewa ndani ya nyumba na Maafisa wa Jeshi la Polisi. Mwili huo ulikuwa umewekwa katika machela na kupakizwa ndani ya gari aina ya Toyota Land Cruiser.



    Kati ya watu waliokuwepo katika mkusanyiko ule uliofika kushuhudia mauaji ya mwanadada, Anita, alikuwepo kijana Don, ambaye alikuwa ni dereva wa bodaboda, aliyekuwa anamwendesha Anita wakati alipokuwa katika shughuli  ya mizunguko yake. Hakika alikuwa na huzuni kubwa kwa vile alikuwa ni mtu wake wa karibu, waliyekuwa wamezoeana.



    “Duh, huwezi kuamini, yaani mwanadada yule ndiyo amekufa?” Mwananchi mmoja akasema kwa masikitiko makubwa kwa jinsi alivyokuwa anamfahamu Anita!



    “Ndiyo, amekufa bwana…” mtu mwingine akadakia.



    “Sijui ni nani aliyemuua?” Kijana mwingine akasema huku akivuta hisia zake juu ya mwanadada huyo mrembo, aliyekuwa anavutia mbele ya macho ya watu.



    “Ni kitu cha kushangaza kwa vile muda siyo mrefu nilimwona akipita hapa…”



    “Aisee, sijui amewakosea nini dada wa watu?”



    “Hivi huyu si anamshikaji wake, yule anayeendesha Harrier?”



    “Ndiyo, huwa anakuja nayo mara kwa mara. Ndiye aliyempangishia nyumba…”



    “Hapana…mauaji haya yana sababu…” Don alisema.



    “Sababu gani?”



    “Unajua Anita alikuwa na bifu na mchumba wake, John Bosho?”



    “Ugomvi gani tena?”



    “John alikuwa anamchukua rafiki yake Anita, na kumfanya mpenzi wake!”



    “Una uhakika?”



    “Ndiyo, nina uhakika na yeye ndiye aliyeniambia…”



    “Basi, inawezekana John andiye aliyemuua?”



    “Inawezekana ndiye.”



    “Utakubali kuwa ushahidi mshikaji?”



    “Sasa ushahidi kwa kitu nisichokuwa na ushahidi nacho?”



    “Hapo ndiyo tatizo…”



    Hatimaye vijana hao walimaliza maongezi yao na kuanza kuendelea kubaki katika eneo hilo, lakini kwa Don, alijua kuwa lazima John Bosho ndiye aliyehusika na mauaji ya mchumba wake, Anita. Hata hivyo, mara baada ya gari lile lililouchukua mwili wa marehemu kuondoka, umati wa watu wote ukatawanyika!



    ********



    NYUMBA moja iliyojengwa mjengo wa kisasa, ilionekana  katika hali ya utulivu wa hali ya juu katika eneo hilo la Kiwalani, jijini Dar es Salaam. Nyumba hiyo iliyokuwa imezungukwa na uzio wa marofali na mbele kukiwa na geti kubwa jeusi, ilikuwani inamilikiwa na mzee Anthony Mkonyi, baba yake mzazi na Anita.



    Kunako majira ya saa kumi na moja za jioni, mzee Anthony Mkonyi, ndiyo kwanza alikuwa ametokea kwenye mihangaiko yake ya kibiashara katika maeneo mbalimbali. Baada ya kuliingiza gari lake aina ya Toyota Prado, ndani ya uzio, akalipaki sehemu ya maegesho. Halafu akashuka na kuingia ndani ya nyumba yake kwa mwendo wa taratibu.



    Wakati huo mke wake, Bi. Matilda alikuwepo akishughulika na kazi ndogondogo za kufanya usafi katika mabanda ya kuku yaliyokuwa nyuma ya nyumba yao. Lakini mzee Anthony hakuwa na shida naye, bali alielekea katika chumba maalum cha mapumziko, ili kuipumzisha akili yake kutokana na mihangaiko ya mchana kutwa. Lakini wakati akielekea chumbani kule, mara simu ya mkononi iliita, akaichukua na kuisikiliza.



    “Haloo…” mzee Anthony akasema.



    “Haloo…Kituo cha Polisi Buguruni hapa…” upande wa pili wa simu ukasema, ikiwa ni simu inayotokea katika Kituo cha Polisi!



    “Unasema kituo cha polisi?” Mzee Anthony akauliza huku akikunja sura yake!



    “Ndiyo, hapa ni kwenye kituo cha polisi…” sauti hiyo ikasisitiza!



    “Ndiyo, niwasaidie tafadhali…” mzee Anthony akasema huku mawazo yake yakiwa yameshatibuka! Mambo ya polisi tena?



    “Natumaini wewe ni mzazi wa Anita Anthony Mkonyi…”



    “Ndiyo, mimi ndiye mzazi wake…”



    “Basi, nakuomba ukaze moyo…”



    “Nikaze moyo? Sjakuelewa…”



    “Ndiyo, mzee…” sauti ile ikasema na kuendelea. “Kuna taarifa siyo nzuri. Mwanao Anita amepata matatizo…



    “Matatizo gani tena?”



    “Ameshambuliwa na mtu asiyefahamika huko nyumbani kwake, Tabata Mawenzi. Hivi sasa amepelekwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili…”



    “Hali yake ikoje?”



    “Ukweli ni kwamba hali ni mbaya…unatakiwa ukamwone!”



    “Oh, ahsante kwa taarifa, nitaenda huko Muhimbili…”



    “Sawa, pole sana…”



    Baada ya kupewa taarifa ile. Mzee Anthony alichanganyikiwa sana baada ya kuambiwa kwamba binti yake ameshambuliwa na mtu asiyejulikana? Je, meshambuliwa kwa sababu gani? Na mpaka muda ule hali yake ilikuwa inaendeleaje huko hospitali alikopelekwa? Hapana, lazima aende haraka sana ili ajue kinachoendelea. Hivyo basi, hakupoteza muda, alitoka mle chumbani na kuelekea kule uani alipokuwa mke wake, Bi. Matilda, akisafisha banda la kuku.



    “Mama Anita,” mzee Anthony akamwita.



    “Bee,” Bi. Matilda akaitikia huku akiacha kusafisha banda la kuku.



    “Hebu njoo kidogo…” mzee Anthony akasema kwa sauti ya unyonge.



    “Sawa, baba…” Bi. Matilda akamwendea taratibu. Akamwona jinsi mume wake alivyohamanika na kuchanganyikiwa, kitu ambacho kilimfanya naye atake kujua kulikoni!



    “Mbona hivyo baba Anita?” Bi. Matilda akamuuliza huku ameshika kiuono chake!



    “Nimepigiwa simu kutoka polisi, kuwa mtoto wetu, Anita ameshambuliwa na mtu asiyejulikana!” Mzee Anthony akamwambia mkewe.



    “Unasema Anita meshambuliwa?” Bi. Matilda akamuuliza!



    “Ndiyo, polisi wanasema kuwa hali yake mbaya, yuko Hospitali ya Muhimbili!”



    “Unasema kweli?”



    “Ndiyo, ni kweli…” mzee Anthony akasema na kuongeza. “Hatuna muda wa kupoteza, twende huko Muhimbili tukamwangalie!”



    “Ni sawa, oh, mwanangu…” Bi. Matilada akasema huku akiweweseka!



    Mzee Anthony na mkewe, Bi. Matilda waliingia ndani na kuvalia harakahara nguo, halafu wakatoka nje na kuliendea gari lao, Toyota Pradao na kupanda. Geti likafunguliwa na mtumishi wa hapo, na mzee Anthony akaliondoa kuelekea katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Waliamua kwenda kushuhudia kuumia kwa mtoto wao, na wala hawakujua kama alikuwa ameshakufa muda mrefu.



            ********



    FOLENI ilikuwa kubwa, hata hivyo ya magari hatimaye wakafika katika Hospitalini ya Taifa ya Muhimbili, na mzee Anthony akalipaki gari katika sehemu ya maegesho, palipokuwa na magari mengine yamepaki hapo. Wakashuka na kuelekea moja kwa moja sehemu ya mapokezi, wanapopokelewa majeruhi wa wanaopata ajali katika sehemu mbalimbali za jiji la Dar es salaam. Hapo palikuwa na wahudumu kadhaa, wakaulizia juu ya Anita.



    Kwa bahati nzuri baada mzee Anthony kufika hapo mapokezi, pia alikuwepo, Kachero Inspekta Malik Mkoba,  ambaye alikuwa akiushughulikia na mwili wa marehemu Anita mara baada ya kuufikisha hapo, kutokea kule Tabata. Na muda huo mwili huo ulikuwa umeshapelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti, baada ya kuthibitishwa na daktari kuwa ameshakufa!



    “Habari za kazi kijana,” mzee Anthony akamsalimia Kachero Inspekta Malik Mkoba.



    “Nzuri, mzee,” Kachero Inspekta Malik akaitikia huku akimwangalia.



    “Mimi ni mzazi wa Anita…” mzee Anthony akasema na kuendelea. “Nimeambiwa kuwa mtoto wangu ameletwa hapa hospitali baada ya kushambuliwa na mtu asiyefehamika…”



    “Oh, pole sana mzee wangu…” Kachero Inspekta Malik akamwambia kwa huzuni huku akimvuta pambeni ili mke wake asiweze kusikia atakachomweleza.



    Baada ya kufika kando kidogo, ndipo alipomalizia kwa kusema, “Wewe ni mzee wetu, na mtu mzima, hivyo haina budi kujikaza kiume!”



    “Ndiyo, kijana, hebu nieleze kitu nikuelewe…” mzee Anthony akamwambia baada ya kuona kama alikuwa anazungushwa!



    “Ni kweli, tumemletwa hapa hospitali muda siyo mrefu, akitokea nyumbani kwake, Tabata Mawenzi, lakini tunasikitika kwamba amefariki dunia!”



    “Unasema binti yangu amefariki?” Mzee Anthony akamuuliza kwa hamaki!



    “Ndiyo, mzee, jikaze kiume. Ameshambuliwa na mtu asiyefahamika majira ya saa tisa za alasiri na hapa ndiyo nataka kuwasiliana na daktari juu ya kuufanyia uchunguzi huo mwili wake…”



    “Oh, Mungu wangu!” Mzee Anthony akasema huku ameshika kichwa chake.



    “Jikaze mzee…” Kachero Inspekita Malik Mkoba akamwambia huku akimshika.



    “Aisee…oh! Naweza kuuona mwili wake?””Mzee Anthony akauliza.



    “Ndiyo, mzee…unaweza kuuona…”



    Wakati huo, mke wake, Bi. Matilda alikuwa amekaa upande wa nje, mbali kidogo na walipokuwa wao. Hivyo basi, asimshtue,  mzee Anthony na Kachero Inspekta Malik walikwenda kuuangalia mwili ule uliokuwa katika chumba cha kuhifadhia maiti, na kumwacha amekaa hapo kwenye benchi upande huo wa mapokezi. Hivyo hakujua kuwa walikuwa wameelekea kwenye chumba cha kuhifadhia maiti, ambacho kiko mbali bna pale.



    Baada ya kufika kwenye chumba hicho, walionana na Daktari Kenedy Mushumbuzi, ambaye ndiye aliyetakiwa kuufanyia uchunguzi mwili huo. Mwili wa marehemu Anita, ulitegemewa kufanywa  uchunguzi jioni ile ile na majibu yake kutolewa kesho yake asubuhi.  Kachero Inspekta Malik na Mzee Anthony waliingia ndani ya chumba cha kuhifadhia maiti, ambapo walifunguliwa droo moja na mhudumu wa hapo, na kuuona huo mwili wa marehemu Anita, na kuhakikisha kuwa ni kweli alikuwa ni mtoto wake wa kumzaa, Anita. Ndipo mzee huyo alipovumilia kama mwanaume, na kupanga cha kumweleza mke wake baada ya kutoka hapo hospitali.



    Kachero Inspekta Malik alielekea ndani ya chumba cha Daktari Kenedy Mushumbuzi, mara baada ya kuachana na mzee Anthony, ambaye kwa muda huo alikuwa ameshachanganyikiwa baada ya kujua kuwa ni kweli binti  yake alikuwa amekufa. Alipoingia ofisini kwake,wakaongea mawili matatu juu ya uchunguzi wa maiti huyo, na baada ya kukubaliana, walipanga kwamba aende kuyachukua majibu hayo kesho yake asubuhi.



    Mzee Anthony alipotoka hapo, alikwenda kuonana na mke wake, Bi. Matilda, ambaye alikuwa amemwacha kule mapokezi. Alimwendea kwa unyonge mkubwa kiasi kwamba alishtuka na kumuuliza:



    “Vipi baba Anita, umepata taarifa gani?”



    “Acha tu…” mzee Anthon akamjibu hivyo.



    “Niache nini sasa? Hali ya Anita ikoje?”



    “Hebu njoo huku tuongee…” mzee Anthony akamwita kando.



    Mzee Anthony na mke wake, Bi. Matilda, walikwenda kusimama kando. Wakati wote huo, Bi. Matilda bado alikuwa na wasiwasi mkubwa sana, kwani alikuwa hajajua hali ya mtoto wake, Anita, inaendeleaje.



    “Vipi baba Anita, mbona tumekuja huku sehemu ya mapokezi, kwa nini tusiulize kama yuko wodini?” Bi. Matilda akaendelea kumuuliza.



    “Turudi nyumbani…” mzee Anthony akamwambia.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Kwa nini turudi nyumbani bila kujua hali ya Anita?”



    “Ndiyo maana nakwambia turudi,” mzee Anthony akamwambia na kuongeza. “Hali ya Anita ni mbaya sana!”



    “Kama ni mbaya, nataka kumwona, kwani yuko chumba cha wagonjwa mahututi!”



    “Ndiyo manaake, huwezi kumwona, turudi nyumbani kwanza!” Mzee Anthony akamdanganya, kwani aliona akimwambia ukweli kuwa alikuwa amekufa, angeanza kupiga makelele hasa ukizingatia alikuwa anampenda sana mtoto wake huyo wa kike.



    Bi. Matilda hakufanya ubishi, alikubaliana naye bila kumwona mwanawe, hivyo wakaondoka pale katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kurudi nyumbani, Kiwalani, huku wakiwa na huzuni kubwa sana!



    ********     



    GETRUDA alizipata rasmi habari za kifo cha Anita baada ya John Bosho kumpigia mara alipotoka kumuua, nyumbani kwake, Tabata Mawenzi. Hata hivyo, kunako majira ya saa mbili za usiku,  alipigiwa tena simu na ndugu za Anita, kumjulisha juu ya kifo hicho, hasa ukizingatia wale walikuwa ni marafiki waliokuwa wamezoeana.



    Hata hivyo, familia hiyo hawakujua kama watu hao wawili walikuwa na mgogoro mkubwa baada baada ya kuchangia mwanaume mmoja, ukizingatia ilikuwa ni siri yao kubwa. Baada ya kupata taarifa hiyo ya pili, ambayo ilimpa nguvu kidogo, Getruda akajiandaa kuelekea huko msibani, ambapo alichukua mkoba wake, ambao aliweka nguo chache kama khanga na vitenge, kisha akaaga majirani zake na kuondoka hapo nyumbani kwake, Ilala, mtaa wa Moshi.



    Getruda akapanda teksi, ambayo ilimpeleka mpaka Kiwalani, nyumbani kwa wazazi wa marehemu Anita. Mara baada ya kufika eneo hilo la Kiwalani, Getruda akamwambia dereva amshushie mbali kidogo na ilipo nyumba ya wazazi wa Marehemu Anita. Na ile ilisababishwa na msongamano wa nyumba zilizojengwa bila mpangilio au kufuata ramani za jiji.



    Eneo lile halikuwa na mitaa iliyowezesha kufika hadi katika nyumba husika. Getruda akashuka katika barabara ya lami iliyokuwa inaelekea maeneo mengine, halafu akamlipa dereva wa teksi. Kisha akaanza kuangalia pande zote na kuona kila mpita njia alikuwa na shughuli zake na wengine wakiwahi kurudi majumbani baada ya kutoka kwenye mihangaiko ya kazi.



    Getruda akaupachika mkoba wake begeni na kuanza kuelekea nyumbani , katika sehemu ile yenye msiba kwa mwendo wa taratibu, wakati huo giza lilishaanza kuingia. Mwili wake ulikuwa mzito, akili imechoka kutokana na kile kifo cha rafiki yake, Anita. Akaendelea kuufuata mtaa ule mdogo na kutokeza pale nyumbani ambapo kwa wakati ule palikuwa pamejaa watu wengi waliofika kwa ajili ya kuwapa pole wafiwa.



    Vilio vya watu waliokuwa wanalia viliweza kusikika, hadi Getruda alipofika na kukaribishwa na watu maalum waliokuwa wamepangwa kwa ajili ya kazi hiyo. Alikaribishwa na kuelekea upande wa wanawake, ambao walikaa sehemu ya ndani. Baada ya kuingia ndani, akakaa kwenye jamvi kubwa lililokuwa limetandikwa ndani ya sebule kubwa, ambayo kwa wakati ule samani zote zilikuwa zimeondolewa.



    Muda wote ule Getruda alikuwa analia kilio cha uchungu, hasa ukizingatia msiba huo ulikuwa unamhusu sana, kwa vile aliyekufa alikuwa rafiki yake, aliyemfananisha na ndugu waliozaliwa tumbo moja. Mbali na hayo, pia mara nyingi walikuwa wakiwatembelea pale nyumbani kuwasalimia wazazi wake, wakiwa wameongozana wote. Sasa mwenzake, Anita ameshakufa!



    Ukweli ni kwamba tukio hilo lilimfanya uchungu uzidi kumwandama moyoni mwake, akalia kwa majuto mpaka machozi yakamkauka. Baada ya kulia vya kutosha, ndipo Getruda aliponyanyuka na kuelekea upande wa pili aliokuwa amekaa mama yake mzazi na marehemu Anita, Bi. Matilda, ambaye alionekana kuwa na huzuni kubwa.



    Kwa muda ule Bi. Matilda alikuwa amejitanda khanga, na alipomwona Getruda, ndipo uchungu ulivyomzidi! Akaanza kulia tena wakiungana na Getruda, wakiwa wamekumbatiana. Walipotosheka kulia, ndipo Getruda alipomwambia kwa sauti ndogo:



    “Oh, mama, pole sana…”



    “Oh, ahsante mwanangu, pole na wewe…Anita ametutoka na sasa hivi amelala ‘Mochwari.’Ametutoka kama mchezo…oh!” Bi. Matilda akasema kwa uchungu mwingi!



    “Pole sana mama…tuwe wavumilivu katika wakati huu mgumu…” Getruda akaendelea kusema.



    “Ni kweli mwanangu…lakini kinachoniuma ni kwamba Anita hakuugua…ameuawa…ni kwa nini?” Bi. Matilda akaendelea kusema.



    “Hilo ndiyo la kujiuliza. Ni kwa nini ameuawa? Na muuaji alikuwa na lengo gani?…Lakini kazi yote tutawaachia Jeshi loa Polisi, ambao wataujua ukweli na muuji atapatikana…” Getruida akaendelea kumfariji Bi. Matida, huku nafsi yake ikimsuta ukizingatia yeye alikuwa anajua chanzo cha kifo cha Anita, muuaji alikuwa ni John Bosho, na pia akiwa ndiye mchangiaji mkuu!



    “Sawa, mwanangu…tutawaachia polisi…” Bi. Matilda akamaliza kusema, halafu akabaki akiendelea kuwaza na pengine akilia. Kamwe hakuna mtu asiyejua uchungu wa mwana, hasa kwa upande wake, ambapo alikuwa ni mtoto wake wa pekee wa kike, ukiacha kaka zake wawili wa kiume!



    Baada ya kumaliza maongezi na kupeana pole, Getruda akaondoka na kwenda kujumuika na waombolezaji wengine, ambao walikuwa wakiongea hili na lile, kila mmoja akisema lake juu ya kifo cha Anita, ili saa zilikuwa zinakwenda.Hata hivyo baada ya muda, simu ya Getruda iliyokuwa kibindoni, ambayo hata hivyo alikuwa ameiondoa mlio, iliita kwa kumtetemesha. Akaichukua na kuangalia namba za mpigaji.



    Ni John Bosho!



    Getruda hakupenda kuisikilizia simu ile pale mbele ya watu wengi, hivyo akanyanyuka taratibu na kutoka nje. Akaenda kuisikilizia mbali kwa kuhofia mtu kuwasikiliza mazungumzo yao ambayo kwa vyovyote yangekuwa nyeti!



          ********



    USIKU huo, John Bosho alikuwa amekaa upande wan je palipokuwa na bustani. Alikuwa anakunywa pombe kali aina ya Jack Daniels, iliyokuwa juu ya meza ndogo mbele yake. Pia, juu ua meza hiyo, palikuwa na glasi ndefu iliyokuwa na pombe nusu. Taa ya nje ilikuwa inawaka mwanga mkali uliomfanya aone kila kitu kilichopo hapo mbele ya nyumba yake ya kifahari.



    Ukweli ni kwamba pamoja na kumuua Anita, lakini nafsi yake ilikuwa inamsuta John, na hofu ikimjia, akiwazia juu ya askari polisi wa upelelezi, ambao mara nyingi hufanya kazi zao kitaalam zaidi  za kumkamata muuaji! Hata hivyo, wakati akiwa katika mawazo hayo, ndipo alioamua kumpigia simu Getruda ili amuulizie yuko wapi!



    “Haloo…John…” upande wa pili Getruda akaipokea kwa sauti ndogo.



    “Uko wapi?”  John Bosho akamuuliza.



    “Niko msibani…nyumbani kwa wazazi wa Anita, Kiwalani…”



    “Oh, umeshafika huko?”



    “Ndiyo, kwani wewe huji huku msibani?”



    “Hapana…siji huko…”



    “Kwa nini?”



    “Nimuue mimi mwenyewe halafu nije?”



    “Ndiyo, lazima uje. Hujui watakutilia mashaka?”



    “Watahisi ni mimi niliyemuua?”



    “Ndiyo manaake…”



    “Kwani ugomvi wetu walikuwa wanaujua? Anita alikuwa msiri sana. Ugomvi wetu ni yeye, mimi na wewe tu, basi! Hivyo ni siri!”



    “Kwa hiyo huji?”



    “Mimi siji, na nimeaga kuwa nimesafiri…”



    “Mama yangu!”



    “Cha muhimu nakusisitiza!” Akaendelea kusema John Bosho. “Usimwambie mtu yeyote, tafadhali tunza siri! La sivyo sikwambii kitakachofuata!”



    “Simwambii mtu!” Getruda akasema huku akiwa na wasiwasi mwingi!



    “Ok, fanya hivyo…kwaheri!” John Bosho akamaliza kusema na kukata simu!



    Baada ya kukata simu, upande wa pili Getruda alibaki amechanganyikiwa. Aliona jinsi John Bosho alivyokuwa anaendelea kumwandama na yeye hata baada ya kumuua rafiki yake Anita. Ukweli ni kwamba aliona hatari iliyokuwa inamkabili, kwani alijua John angemdhuru kweli kama angeitoa ile siri kwa mtu yeyote!



    Sasa afanyeje?



    Ukweli ni kwamba Getruda hakuwa na la kufanya zaidi ya kuutia mdomo wake kufuli! Na mara baada ya kumaliza kuongea na John, akajiondoa  na kurudi kuungana na waombolezaji wengine. Akajumuika nao katika maombolezo huku nafsi yake ikimsuta ukizingatia mkasa mzima alikuwa anauelewa.Na yeye alikuwa mhusika mkuu!



    Baada ya kumaliza kuongea na Getruda, John Bosho alibaki akiiangalia ile simu yake. Halafu akaiweka juu ya meza na kujiegemeza kwenye kiti cha mbao kilichokuwa nje ya nyumba yake sehemu hiyo ya kibarazani, karibu na bustani. Alikuwa amekaa hapo kwa muda mrefu huku akitafakari juu ya mauaji yale ya mchumba wake, Anita aliyoyafanya.



    John Bosho alikumbuka kuwa wakati akitekeleza mauaji yale kule ndani ya bafu la kuogea, hakuweza kuacha alama zozote za vidole, ambazo hutumika kama ushahidi, zaidi ya lile bomba la sindano na bahasha aliyonunua. Hata hivyo, hakuridhika na lile bomba la sindano aliloliacha mle bafuni, kwani lingemletea matatizo hasa wakifuatilia katika duka alilonunua  katika duka la dawa, pale Aroma, Tabata. Sasa afanyeje? Hakuwa na la kufanya zaidi ya kujifariji!



    Hata hivyo, John Bosho aliendelea kunywa pombe kwa wingi huku akiangaza macho yake pande zote za himaya ya nyumba yake ile ya kifahari, ambayo kwa muda ule ilikuwa imepooza. Mle ndani ya nyumba hiyo, walikuwa wao wawili tu, yeye pamoja na mlinzi wake mmoja wa jamii ya Kimasai, ambaye kwa muda ule alikuwa akizunguka eneo zima ili kujionyesha kwa bosi wake, kuwa alikuwa anawajibika kikazi.



    Pia, mlinzi huyo alikuwa akimvizia John Bosho ampe angalau pombe kidogo anywe, kitu ambacho alikuwa anafanya mara kwa mara anapokuwa amefurahi. Lakini kwa siku ile, hakuwa na furaha yoyote, alikuwa na huzuni kubwa, hivyo hakuwa na muda wa kuchangamkiana na huyo mlinzi, ambaye muda huo alikuwa amejitanda lubega lake la rangi nyekundu. Kwanza kabisa, alikuwa anawaza sana juu yake, kama anaweza kupambana na maswali ya kipolisi endapo wangefika kumhoji baada ya kumshtukia.



    Wasiwasi ulimpata John kiasi kwamba alipanga kuwa ni lazima ambadilishe haraka sana mlinzi huyo wa kimasai na kumweka mlinzi wa kampuni ya binafsi aliyepitia mafunzo ya ulinzi. Alipanga kuwa kesho yake tu, atawasiliana na kampuni moja ya ulinzi, iliyoko katika eneo la Ukonga Banana, ambayo itampatia mlinzi wa kulinda hapo kwa mkataba maalum



    Baada ya kuona hapewi chochote na tajiri yake, yule mlinzi aliondoka eneo hilo na kuhamia sehemu nyingine ya lindo lake. Akamwacha John Bosho akiendelea kunywa pombe ile taratibu hadi alipokuwa chakari, akajilaza palepale nje, kwenye kibaraza sehemu iliyokuwa na upepo mwanana. Hatimaye alikuja kushtuka kwenye majira ya saa nane za usiku, ndipo alipojikokota na kuingia ndani kulala!



    ********



    MAJIRA ya saa nne na nusu za asubuhi, ilimkuta  Kachero Inspekta Malik Mkoba akiwa barabarani, kuelekea katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, ili kupata taarifa ya Daktari Kenedy Mushumbuzi, aliyeufanyia uchunguzi mwili wa marehemu, Anita, jana yake mara baada ya kufikishwa hapo.



    Mwili huo ulitakiwa ufanyiwe uchunguzu haraka ili ibainike ni kitu gani kilichomdhuru, au kama ni sumu, je, ni sumu ya aina gani iliyosababisha kifo chake. Huo ni utaratibu wa kawaida kabisa wa kipolisi, kabla ya mwili huo kukabidhiwa kwa familia yake tayari kwa maziko.



    Kachero Inspekta Malik Mkoba aliamua kutumia gari lake la binafsi, aina ya Nissan Laurel, kutokana na uhaba wa magari ya polisi hasa wakati wa dharura kama zile, ambazo huwa zinatokea katika maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam. Asubuhi hiyo alikuwa amevalia nadhifu, suti yake ya rangi nyeusi, shati jeupe na tai ya rangi nyekundu liyochanganyika na bluu. Hakika alipendeza sana na kuonekana ni kijana anayejipenda.



    Ingawa magari yalikuwa ni mengi barabarani na yaliyosababisha foleni kubwa, Kachero Inspekta Malik Mkoba alifanikiwa kufika katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, halafu akalipaki katika sehemu ya maegesho. Kisha akashuka na kuelekea ndani ofisi, iliyoko jirani chumba cha uchunguzi wa maiti, ambapo alimkuta daktari yule aliyeufanyia uchunguzi mwili wa mwanadada, Anita. Alikuwa ni Dokta Kenedy Mushumbuzi, ambaye ni mtaalam na maalum kwa kazi  zile za uchunguzi wa maiti zilizokuwa na utata, zinazohusiana na Jeshi la Polisi.



    Muda ule Daktari Kenedy Mushumbuzi alikuwa ndani ya ofisi yake nadhifu na safi, amekaa kwenye kiti cha mzunguko, nyuma ya meza yake akiandika taarifa fulani hivi. Wakiwa ni watu wanaofahamiana sana katika shughuli zao za kikazi, daktari huyo alimkaribisha Kachero Inspekta Malik Mkoba kwa ukarimu.



    “Karibu Inspekta Malik…”



    “Ahsante sana Dokta Mushumbuzi…” Kachero Inspekta Malik akasema huku akikaa kwenye kiti kilichokuwa mbele ya meza yake.



    “Natumaini umekuja kupata taarifa za uchunguzi wa mwili wa marehemu, Anita ulioletwa hapa jana jioni…” Daktari Kenedy Mushumbuzi akamwambia huku akiirekebisha miwani yake mieupe.



    “Ndiyo, Dokta, nimeifuata ripoti hiyo. Si unajua tena kazi zetu, nataka kuanza upelelezi mara moja!” Kachero Inspekta Malik akasema.



    “Hakuna tatizo,” Daktari Kenedy Mushumbuzi akasema. Halafu akalifungua kabati moja na kutoa faili ambalo aliliweka pale mezani na kulifungua. Akaendelea kusema, “Nimeufanyia uchunguzi mwili ule na kugundua marehemu amekufa baada ya kudungwa sindano iliyokuwa na sumu kali sana, ambayo ina uwezo wa kuua haraka sana kwa kusimamisha mapigo ya moyo…” Daktari Mushumbuzi akanyamaza kidogo huku akimwonyesha Inspekta Malik ile taarifa.



    “…Sumu hiyo ilifanya damu igande na kusababisha mapigo ya moyo yasimame. Hivyo basi, kutokana na hali hiyo, ndiyo maana mwili wa marehemu umevimba sana kiasi cha kubadilika rangi na kuwa mweusi. Pia, nimegundua kuwa marehemu alibakwa kabla ya kuchomwa ile sindano ya sumu; kwa sababu katika sehemu zake za siri kumekutwa mbegu za kiume. Nafikiri umenipata vizuri Inspekta Malik, kwa taarifa hii!”



    “Nimekuelewa vizuri Dokta. Tunashukuru sana kwa ushirikiano, ambao utatusaidia katika upelelezi wetu,” Kachero Inspekta Malik akasema.



    “Basi, huo ndiyo uchunguzi nilioufanya. Hivyo mwili wa marehemu unaweza kuchukuliwa na ndugu zake kwa ajili ya maziko. Pia, taarifa zote za uchunguzi wa kifo chake watazipata…” Daktari Fabian Mushumbuzi akaendelea kusema huku akichambua makaratasi yenye taarifa ile.



    Baada ya Kachero Inspekta Malik kupata taarifa zile za kifo cha Anita, akamuaga Daktari Mushumbuzi na kuondoka, huku akisindikizwa naye hadi nje ya ofisi yake ambapo walipeana mikono na kuagana. Malik akaliendea gari lake na kupanda, halafu akaliotoka eneo lile la Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, kuelekea ofisini. Muda wote alikuwa na mawazo juu ya yule mtu aliyefanya mauaji yale ambapo kwa muda ule alikuwa hajamgundua kama ni mtu hatari, John Bosho!



    Vilevile Kachero Inspekta Malik alijiuliza kwamba muuaji yule alipitia wapi na kufanya mauaji yale ya kinyama na hatimaye kumbaka marehemu Anita mle mle! Na pia alitoka vipi wakati wapangaji wa nyumba ile waliwahi kutoka nje baada ya kusikia makelele yale ya kuomba msaada na kwenda kusimama karibu na mlango wa bafu, ambao nao ulikuwa haujafungwa kwa ndani! Kwa vyovyote alijua ni mtu hatari sana!



    Hatimaye Kachero Inspekta Malik alifika kituoni na kuingia ofisini kwake. Baada ya kukaa, kitu cha kwanza kukumbuka, ni ile bahasha ndogo aliyoikuta ndani ya bafu, ambapo ndani yake palikuwa na lile bomba la sindano. Jana yake aliiweka ndani ya droo yake mara baada ya kurudi kutoka Tabata lilipotokea tukio lile la mauaji, hivyo akaifungua droo na kuitoa ile bahasha ambayo alianza kuikagua kwa makini na kuiona ilikuwa ya kawaida tu, iliyokuwa na maandishi ya muhuri yaliyosomeka ‘Kishada Medics.’



    Baada ya kumaliza kuisoma, akairudisha ndani ya droo, ikiwa na lile bomba la sindano ndani yake. Kachero Inspekta Malik akaona kuwa lilikuwa ni jambo la busara kuuanza upelelezi wake katika lile duka la dawa, lililokuwa eneo la Tabata Aroma. Ni duka lililokuwa linauza madawa baridi ya binadamu, ambalo linajulikana sana, ukizingatia liko sehemu ya wazi tu. Kwa vyovyote ilionekana kwamba muuaji yule alikuwa amenunua lile bomba la sindano kwenye duka lile wakati alipokuwa anakwenda kutenda unyama dhidi ya mwanadada Anita!



    Hata hivyo, Kachero Inspekta Malik aliendelea na kazi nyingine zilizokuwa zinamkabili, kiwa ni pamoja na kuyashughulikia mafaili kadhaa ya makosa mbalimbali. Wakati akiendelea na kazi, pia, alipanga kuwa ni lazima ahudhurie mazishi ya marehemu Anita, yaliyotegemea kufanyika kesho yake jioni, nyumbani kwao, Kiwalani. Kwa vyovyote alijua kwamba asingekosa kupata mambo mawili matatu yatakayoweza kumsaidia katika upelelezi wake, kwani kifo kile kilikuwa na utata mkubwa uliokuwa umemweka njiani panda!.



    ********         



    SHUGHULI za mazishi zilikamilika, ambapo marehemu Anita alizikwa siku ya tatu yake jioni, katika makaburi ya Kiwalani, na maziko hayo yaliyohudhuriwa na watu wengi, wakiwa ni wakazi wa Kiwalani, ndugu jamaa na marafiki, pia akiwemo rafiki yake, Getruda. Huzuni ilitawala kote kutokana na kifo kile cha kutatanisha kilichowaacha watu njia panda bila kujua muuaji ni nani.



    Vilevile walikuwepo ndugu, jamaa na marafiki, bila kukosa Kachero Inspekta Malik Mkoba. Yeye alihudhuria pale bila mtu yeyote kumshtukia katika eneo la msiba, kwani alijaribu kuvalia mavazi yaliyombadili kidogo, na kuonekana ni mmoja wa watu wanaohusika na msiba huo kwa namna moja ama nyingine.



    Lakini cha kushangaza ni kwamba mtu aliyekuwa mchumba wake, John Bosho, hakuhudhuria katika msiba ule ingawa ulimhusu sana, ukizingatia marehemu Anita alikuwa mchumba wake walioahidiana kuoana. Baada ya kumaliza kuzika, watu wakatawanyika na kubaki baadhi ya ndugu, na muda wote kachero Inspekta Malik alikuwa akijiuliza juu ya kutomwona, ingawa alikuwa ametajwa kwenye risala iliyosomwa pale makaburini.



    Baada ya kumalizika kwa mazishi hayo ya mwanadada, Anita Anthony, wazazi wake waliamua kukaa kikao cha faragha hapo nyumbani kwao, Kiwalani, ambapo walikuwa wanajadili juu ya John Bosho, mchumba wa Anita kutokufika kwenye msiba mara baada ya yeye kuuawa na mtu asiyejulikana. Kamwe haikuwaingia akilini kuwa, kuwa, mtu aliyekuwa ameshajitambulisha na anatambulika na familia nzima, halafu asifike kwenye msiba kwa kusema eti amesafiri? Hiyo inaingia akilini kweli?



    “Hivi mke wangu, unafikiria nini juu ya John Bosho, aliyekuwa mchumba wa marehemu mwanetu, Anita?” Mzee Anthony alimuuliza mkewe, Bi. Matilda.



    “Hata mimi nashangaa, sijui inakuwaje mchumba wake amekufa halafu yeye haonekani katika msiba, mpaka anazikwa?” Bi. Matilda akasema huku akitikisa kichwa chake!



    “Tokea msiba umetokea, nimejaribu kumpigia simu, lakini hapatikani. Na mara ya mwisho nilimpata lakini akasema kuwa yuko safarini nje ya jiji la Dar es Salaam…” Mzee Anthony akasema huku amechukia.



    “Hivi inawezekana mtu afiwe na mchumba wake lakini ashindwe kufika kwa ajili ya safari? Si anahairisha na kurudi haraka? Safari ina umuhimu kuliko maisha ya binadamu kweli?”Bi. Matilda akaongeza kusema.



    “Hata mimi sipati jibu,” mzee Anthony akasema kinyonge.



    “Jambo la muhimu ni kuwasiliana na Jeshi la Polisi, kwani inawezekana akawa ni mtuhumiwa namba moja,” Bi. Matilda akasema na kuongeza. “Ni kweli kabisa, mimi ninawasiwasi na mwanaume huyo, kamtoa kafara mwanetu ili aimarishe utajiri wake!”



    “Itabidi tufanye hivyo, mpigie simu aje hapa nyumbani.”



    Mzee Anthony alimpigia simu Kachero Inspekta Malik Mkoba, na kumwomba wakutane katika kujadili suala lile. Malik ambaye ndiye mpelelezi wa suala lile, hakukawia kufika mara moja pale nyumbani, Kiwalani. Baada ya kufika alikaribishwa vizuri, ambapo walitafuta sehemu nzuri na kuanza kuongea kwa kina.



    “Ndiyo mzee wangu, nimeitikia wito wako…” Kachero Inspekta Malik akasema.



    “Nimekuita Inspekta, juu ya kifo hiki cha mwanangu, Anita, unajua kina utata kidogo….” mzee Anthony akasema.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ndiyo, ni kifo chenye utata, ndio maana tunataka tumjue muuaji!” Kachero Inspekta Malik alimwambia.



    “Lakini kuna kitu kimoja kinanishangaza. Kuna huyu mtu anayejiita mchumba wake, ambapo tokea mwanangu amefariki na kuzikwa, hajafika hapa nyumbani…”



    “Ni kwa nini hajafika msibani?”



    “Hata sisi tunashangaa wakati Anita alikuwa mchumba wake! Hivyo kwa namna moja ama nyingine namtilia shaka kuhusika na kifo hicho!”



    “Kwani walikuwa na ugomvi?”



    “Kama walikuwa na ugomvi sielewi, lakini mara nyingi walikuwa wakitofautiana kutokana na uchelewaji wa masuala ya kufunga ndoa…”



    “Sasa hicho unahisi hicho ndicho kilichosabaisha mauaji?”



    “Ndiyo maana nikakuomba uje. Unaweza kutusaidia kwa hilo, ukimpata John Bosho, unaweza kuupata ukweli wa haya yote tunayojiuliza,” mzee Anthony akaendelea kumwambia Kachero Inspekta Malik Mkoba.



    “Hakuna wasiwasi mzee, nitafanya hivyo. Nitamtafuta John Bosho na kumhoji kuhusu hilo, na kama akibisha nitamkamata na kumhoji akiwa chini ya ulinzi!” Kachero Inspekta Malik Mkoba akamwambia mzee Anthony.



    Baada ya maongezi yale kumalizika,  Kachero Inspekta Malik aliaga na kuondoka pale nyumbani kwa mzee Anthony, Kiwalani. Kichwani mwake alipanga kumtafuta John Bosho kwa hali na mali, ili aweze kufanya mahojiano naye ya kina, huenda akaambulia chochote juu ya mauaji ya mwanadada, Anita. Hata hivyo, aliamua kumweka kiporo, ili amfuatilie nyendo zake kujua alikuwa na agenda gani za siri!



            ********



    WAKATI watu wanaendelea na shughuli za mazishi ya mwanadada, Anita Anthony, John Bosho likuwa ana mipango yake mingine kabisa, akitapatapa katika kutaka kujinasua katika tuhuma za mauaji ya mchumba wake huyo ambaye alikuwa hana hatia yoyote. Kivuli cha Anita kilikuwa kinamsumbua sana, na kuanza kujutia mara dufu!



    Siku hiyo John Bosho hakushinda nyumbani kwake, Ukonga. Alikuwa amekwenda Chamazi, nyumbani kwa mganga mmoja wa jadi, aliyejulikana kwa jina la mzee Chiloto Bandua, ambaye ni mtu aliyekuwa anawasaidia sana katika shughuli zao haramu. Mganga huyo aliaminika kuwa alikuwa na uwezo wa kutengeneza dawa za mazindiko, ambazo pia zinaweza kukufanya usiweze kutambulika kama umefanya uhalifu .



    Sababu kubwa iliyokuwa imempeleka kwa mzee Chiloto Bandua, ni juu ya kupata ushauri baada ya kutekeleza mauaji yale ya mchumba wake, Anita, ili ampatie dawa zitakazomfanya asikamatwe na Jeshi la Polisi, ambao kwa vyoyote watakuwa wameshaanza upelelezi wao. Ukweli ni kwamba ni mara nyingi mganga huyo aliweza kuwapatia dawa nyingi, ikiwa ni pamoja na ya kujizindika mwilini, katika azma ya kutimiza kazi zao za ujambazi.



    Tuseme ni kwamba, kabla ya wao kwenda kufanya kitendo cha uhalifu eneo fulani, ilikuwa ni lazima wapatiwe dawa maalum na mganga huyo, kwa ajili ya kujizindika mwilini na hata katika silaha zao watakazotumia, kwa kile walichoamini kuwa kingewasaidia kutimiza malengo yao bila kukamatwa, kwa vile polisi wasingeweza kuwaona kamwe! Ni giza tupu!



    Hivyo basi, siku hiyo John Bosho akitumia gari lake, Toyota Harrier, aliondoka nyumbani kwake kuelekea huko Chamazi, wala hakujali chochote kuwa siku ile ndiyo kulikuwa na mazishi ya marehemu Anita, aliyekuwa mchumba wake. Tokea mwanzo alikuwa ameshapanga kutohudhuria, ukizingatia yeye ndiye muhusika mkuu wa mauaji. Hata hivyo, alijua kuwa habari za mazishi hayo atazipata kwa Getruda, ambaye alikuwa amekwenda kuhudhuria msiba ule tokea jana yake.



    Hatimaye baada ya kusumbuana na foleni ya magari barabarani, katikati ya jiji, John Bosho alifika katika Barabara ya Kilwa, ambayo aliifuata hivyo ambayo haikuwa na usumbufu wa foleni. Hatimaye alifanikiwa kufika Chamazi, nyumbani kwa mganga, mzee Chiloto Bandua. Akalipaki gari lake mbali kidogo na nyumba ile, halafu nusu iliyobaki akatembea kwa miguu hadi alipofika eneo husika, ambapo alipokewa vizuri na kukaribishwa kama mteja wa kawaida aliyekuwa amezoeleka pale.



    Wote wawili waliingia ndani ya chumba maalum kinachohusika na shughuli za uganga, kilichokuwa kando ya nyumba yake kubwa. Baada ya kuingia katika chumba kile cha uganga, ambapo yeye alipokewa na harufu nzito ya dawa za mitishamba, mavumba, pamoja na udi. Kwa kiasi fulani haikumpendeza, lakini hakuwa na la kufanya hasa ukizingatia alikuwa amekwenmda kuganguliwa.



    Hivyo basi, wakakaa kwenye jamvi lililokuwa limetandikwa karibu nusu ya chumba kizima kilichokuwa tupu bila viti. John Bosho hakupoteza muda, akamweleza mzee Chiloto Bandua juu ya jambo lililompeleka hapo nyumbani kwake.



    “Mzee wangu, nimekuja kwako tena…” John Bosho akamwambia mganga huyo.



    “Karibu sana, bwana mdogo…” mzee Chiloto Bandua akamwambia huku akimwangalia kwa makini.



    “Huko nilikotokea nimeharibu mzee wangu!”



    “Umeharibu nini?”



    “Nimeua!” John Bosho akasema na kuendelea. “Mbaya zaidi nimemuua mchumba wangu mwenyewe, si unaona kazi hiyo?”



    “Umemuua mchumba wako? Siyo kusaka fedha tena kutoka kwa matajiri?”



    “Ndiyo, nimemuua kwa sababu alikuwa anataka kunichoma kwa polisi. Sasa huoni kama lilikuwa ni jambo la hatari sana kwa upande wangu na kwako pia?”



    “Ni kweli kabisa, huyo mchumba wako alikuwa hakutakii mema. Kwa hiyo unatakaje?”



    “Ninataka unitengenezee dawa nisoweze kukamatwa na polisi…maana najua saa hizi wako mbioni kumsaka muuaji!”



    “Aisee, kweli kuna kazi…” mzee Chiloto Bandua akasema huku ameshika kidevu chake. Alimwelewa na kuona kuna haja ya kumpatia ufumbuzi wa suala lile, ingawa pia kwa upande wa pili aliona ni suala zito sana. Lakini akiwa ni mganga asiyependa kushindwa, na shida yake ikiwa ni fedha, akaamua kumpa ushauri wa uongo!



    Mzee Chiloto Bandua akavuta pumzi ndefu na kusema kwa sauti ndogo lakini yenye msisitizo, “Ndiyo bwana mdogo…nimekuelewa vizuri. Si unasema unataka dawa ya kufanya usikamatwe na Jeshi la Polisi?”



    “Ndiyo hivyo mzee…hakuna jingine!”



    “Dawa nitakupa. Lakini…” mzee Chiloto Bandua akasema na kusita.



    “Lakini nini mzee?” John Bosho akamuuliza huku amemkazia macho!



    “Kuna masharti kidogo…”



    “Masharti gani? Naomba unieleze…”



    “Nitakueleza kijana wangu…usiwe na wasiwasi. Natumaini unaelewa kuwa dawa zangu ni kiboko!”



    “Lazima niwe na wasiwasi, si unajua nimeua mtu mzee? Na pia ndiyo maana sisi tunakuja kwako, na kazi nyingi tumefanikiwa bila matatizo yoyote!”



    “Sawa, ili usiweze kukamatwa na Jeshi la Polisi, ninakupa kazi moja ngumu kidogo. Lakini ndiyo suluhisho ya tatizo linalokukabili…”



    “Kazi ngumu?”



    “Ndiyo…”



    “Hebu niambie kazi hiyo.



    “Ni kwamba, ili ufanikiwe kukwepa kitanzi hicho, inakubidi ufanye kazi ya ziada. Ukafukue kaburi alilozikwa mwanamke uliyemuua!”



    “Mh, unasemaje” John Bosho akaguna baada ya kusikia kuwa alifukue lile kaburi la Anita.



    “Unaguna hata sijakueleza?” Mzee Chiloto Bandua akamwambia na kuendelea. “Basi naona kuwa wewe huna shida ya kupata dawa!”



    “Nataka mzee…” John Bosho akasema huku akijifanya kuufukuza ule woga wa kulifukua lile kaburi la Anita!



     Na kweli ilitisha!



    “Basi,” mzee Chiloto Bandua akaendelea. “Baada ya kulifukua hilo kaburi, mtaitoa ile maiti ndani ya sanduku. Baada ya kuiondoa maiti hiyo, mtazikata baadhi ya sehemu za siri kwa kuzinyofoa, kisha ziletwe hapa kwangu haraka sana, tayari kuzifanyia dawa ambayo itakayofanya usikamatwe wala kuhisiwa na Jeshi la Polisi kama wewe ni mhusika mkuu wa mauaji ya mchumba wako!”



    “Nimekuelewa mzee, lakini…” John Bosho akasema huku wasiwasi ukiongezeka.



    “Lakini nini kijana? Naona kama wewe huna haja ya kufanikiwa!” Mzee Chiloto bandua akamwambia kwa ukali kidogo!



    “Masharti magumu kidogo mzee…”



    “Ugumu wake nini bwana mdogo?”



    “Kulifukua kaburi…ninaweza kushtukiwa na wakazi wa eneo lile!”



    “Hilo siyo sharti gumu! Je ningekwanbia ukamchinje mwanao, mkeo au mama yako mzazi?”



    “Mh, na hiyo ni kali zaidi!”



    “Basi hilo ni sharti dogo!”



    “Sawa mzee, Nitafanya hivyo!”



    “Baada ya kuniletea viungo nilivyokutuma, mambo yatakuwa mazuri. Nakuomba uzingatie hilo!” Mzee Chiloto Bandua akaendelea kumsisitiza John Bosho, ambaye alimwelewa vizuri. Lakini ukweli unabaki kuwa alikuwa na wasiwasi mkubwa!



    Baada ya makubaliano yale, John Bosho na mzee Chiloto Bandua wakaagana, yeye akapanda gari lake na  kuondoka pale Chamazi, kurudi jijini. Njia nzima alikuwa akiendesha gari, na mawazo mengi sana yakimkaba kichwani mwake, akiwazia kama kazi ile ya kuufukua mwili wa Anita kama itafanikiwa, na katika masharti yote aliyokuwa anapewaga na mganga yule, yale yalikuwa kiboko!



    Alipofika nyumbani kwake, Ukonga, John Bosho alijimwagia maji ya baridi, kiasi kwamba mwili wake ulipata nguvu. Halafu akakaa na kuwapigia simu vijana wake wawili wa kazi, Chikwala na Robi, ambao ni kati ya vijana wengine, Muba, Kessy na Chogolo, ambao aliwaambia na kuwa kesho yake wakutane katika kikao cha dharura.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ahadi hiyo ilikuwa ni ya kukutana  ndani ya bohari la siri lililoko eneo la  Ubungo Machimbo ya Mawe, ili wapange mikakati ya kazi iliyokuwa inawakabili mbele yao. Vijana hao, ambao wako makini sana, walimwelewa bosi wao, na kuahidi kukutana kwa muda muafaka kama walivyokubaliana!



          ********







    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog