Search This Blog

Monday 24 October 2022

KIMBIA, KIMBIA! [RUN NIGGER, RUN!] - 1

 

     IMEANDIKWA NA : HUSSEIN KULINDWA



    *********************************************************************************





    Simulizi : Kimbia, Kimbia! [Run Nigger, Run!]

    Sehemu Ya Kwanza (1)



    MARA baada ya kumaliza kupata chakula cha mchana, alielekea chumbani kwake kujipumzisha. Huko alipumzika kitandani huku akiwa amefungulia radio yake na kusikiliza mziki laini huku akisoma moja ya magazeti yaliyokuwepo hapo kitandani kabla ya kuingia kwake chumbani humo.



    Na ndivyo si zaidi ya dakika arobaini, tayari alichotwa na usingizi ambao hatahivyo ulimlaza hadi majira ya jioni.

    Aliamka, akatoka chumbani na kuingia sebuleni ambako nduguze walikuwa wakiangalia sinema (Unfaithful); na huku akisalimiana nap, alijiunga katika utazamaji wa filamu hiyo.

    Hata hivyo, hakuweza kuiangalia sana filamu hiyo; na hivyo, hakufanya kwa sababu tu ladha ya kutamani kuitazama ilichafuliwa na kule kukerwa na mazungumzo ya nduguze ambao walikuwa wakizungumzia mambo ya wanaume (pengine mabwana zao) kwa kulinganisha na sinema hiyo; bali hivyo alitokana pia na ukweli picha hiyo ilianza kumchosha sana kutokana na kuirudia kuitazama mara kadhaa huko nyuma.

    Hivyo ndivyo kwa kiwango fulani alivamiwa na upweke uliopewa makucha ya kuukwaruza moyo wake kutokana na hizo zungumza za dada zake; na ndivyo hali hiyo ya kujihisi mpweke ilisababisha ajikute akiwakumbuka watoto zake mapacha ambao alikuwa hajawatia machoni kwa takriban mwezi mzima na nusu hivi.



    Mawazo hayo yalimchukua hadi kumfikisha katika kujiundia uamuzi ya kwenda kule mbagala ambako ndiko watoto wake walikuwa wakiishi pamoja na mama yao mzazi.

    Hivyo, aliinuka na kuondoka sebuleni bila hata ya kuwaaga dada zake. Alirudi chumbani kwake na kuvua nguo na kisha alivaa bukta, akatungua taulo na kutoka kuelekea maliwatoni.

    Haikumchukua dakika nyingi kuoga; na alipomaliza, alitoka bafuni na kisha akarudi chumbani tayari kwa kujibodoa na kuvaa.

    Mara baada ya kuvaa, aliondoka chumbani na kuelekea jikoni ambako alimkuta mama yake aliyekuwa kajituliza kitini huku msichana wa kazi akiwa amekaa mkekani akikatakata nyama.

    Alisimama nyuma ya kiti hicho alichokikalia mama yake akikiegamia.

    Alitulia kidogo hapo kuruhusu kuzivuta pumzi; mama yake bado hakujua ingawaje msichana wa kazi alijua kwani alimuona.



    “Mama, nina shida.”

    Mama Esta alishtuka kidogo na kisha aligeuza kichwa chake nyuma, na alipomuona sauti ndogo ya kuguna ilimtoka!

    Ndio, bila mama yake kumtazama ingekuwa shida kiasi kumjua kutokana na wanawe kufanana sauti, tena wakifanana na sauti yake!

    Naam, huyu aliitwa Henry Kipekecho, mtoto wa pekee wa kiume katika familia yao ambaye licha ya kufanana na baba yake, alikuwa na sauti ya kike iliyokuwa nyororo kiaina! Kwamba, sura na sauti yake havikuendana kabisa, kwani ilikuwa ni sawa na kujaribu kuwafananisha paka na panya! Hasa ukizingatia kuwa Baba Esta alikuwa na sura mbaya kiasi, basi ndivyo pia Henry alikuwa hivyo bila kujumlisha ile ‘pasi ya matako’ iliyozidi kumfanya alandane sana na baba yake!



    Mama Esta aliacha tena kumtazama kabla ya kutoa jibu, “nitaongeaje na mtu mgongoni? Hiyo ni adabu?”

    Henry alijilamba midomo kidogo, na kisha akatoka nyuma ya kiti; alisimama mbele ya mama yake na kuanza kusema, “mama, nataka kwenda kuwaona wanangu. Sijawaona muda mrefu!”

    “Nani kakukataza?...kwanza tangu lini ukaniaga unaenda huko?....Wewe sema unachotaka kusema! Acha vunga za kipuuzi hapa...Mtu mzima ovyoo!”

    “Sasa mama....?” Henry hakumalizia usemi aliotaka kuusema; na usoni tayari mistari miwili mitatu hivi ilianza kuelekea kutaka kujitokeza.

    Baada ya sekunde chache aliendelea tena, “mama…yaani, unani...aah! Anyway, siyo mbaya sana kwani haya yote ni kweli ni kwa ajili ya upuuzi wangu mwenyewe.”

    Mama Esta hakujibu.



    Henry alivyoona mama yake bado hajibu, alisema tena huku akifanikiwa kuondoa ile mistari iliyojichora katika paji lake la uso, “mama, nilikuwa naomba nauli, nataka kutoka kidogo.”

    “Aha, kumbe ulikuwa unaomba! Isipokuwa kwa sasa…baba huombi, eeh?” Mama Esta alimjibu kwa kuzungumzia puani kwa namna ya kumdhihaki na kisha aliendelea kusema, “hivi kwanini hutulii ukatulizana? Au nyumba hii ina miba inakuchoma?”

    Mama Esta alitoa cheko dogo.

    “Sio hivyo mama!”

    “Sio hivyo!” Sauti ya puani ilimtoka tena mama Esta huku ikisaidiwa na mkono wake wa kushoto kubana pua zake. Zaidi alisema, “kumbe nini?”

    “Ahm…nataka kuwaona…nataka kwenda kuwaona watoto wangu kama nilivyokueleza.” Henry alisema huku vidole vya mkono wa kulia vikichezeachezea ndevu zake za kidevuni.

    ‘Kubwa jinga na kigari chako mshenzi!’ Henry alihisi kuisikia sauti fulani ikimkoromea mawazoni.

    “Nani atakuweza kwa uongo? Hizo ndizo fix za leo, sivyo?” Mama Esta alimjibu baada ya kutoa mguno mwingine mdogo wa kebehi. Aliendelea kusema, “we sema unataka kwenda kwa huyo mwanamke wako! Nani asiyekujua bwana!”

    “Mama bwana…aah!” Henry alisikitika kinamna.

    “Salma! Ebu nipe hiyo pochi hapo juu ya hilo jiko.” msichana wa kazi, aliagizwa. Hakuwa mbali na jiko. Aliinuka na kuunyoosha kidogo mkono wake wa kulia; na kisha ndipo aliweza kuikamata pochi.

    Mama Esta akapewa pochi.

    “Haya shika.” Alipatiwa noti ya alfu kumi.

    Henry aliipokea noti ile ingawaje lile tabasamu lake lililokuwa limeanza kuchipuka kwa kuchezacheza hapo mdomoni mwake lilianza tena kuchuja; ndio, hakuridhishwa na kupewa kiasi kile.

    “Mama, huyu msimbazi ni ponyoo dhaifu, hawezi kupenyee. Niongezee angalau mdogo wake…hapo wanaweza kusaidia kuzungumza vizuri. Mama si wajua mambo ya kasi mpya ari mpya?.”

    “Sikuelewi, wasemaje?” Mama Esta alimaka.

    Akijiumauma, Henry alijibu, “mama niongezee japo alfu tano hivi. Hii kumi haitoshi.”

    “Leo hali siyo njema.” Mama Esta alisema huku akichambua noti kadhaa zilizokuwemo katika pochi yake. Baadaye, alimpatia noti tatu za alfu huku akiendelea tena kusema, “haya, kama kweli wewe ni mwanaume niletee wajukuu!”

    Henry hakujibu; alitumbua macho!

    Hata hivyo, angejibu nini na wakati kila mara husisitiziwa jambo hilo na asiweze kulitenda! Kwa upande mmoja alimuona mama yake kama aliyemkashifu, lakini; na wakati kwa upande mwingine, huko aliyaona maneno yake yakisimama ni ukweli ukumbushao hadithi tupu imuumizayo.

    ‘Kweli mtu na tafsiri zake!’ Aliishia kujisemea.

    “Hivi nasema na nani hapa?” Mama yake alimkazia macho. Alizidi kufoka tena, “Hivi wewe vipi lakini? Kwanini huwi ngangari kuwachukua watoto wako na wakati haki zote unazo? Walete watoto, tutawalea bila matatizo kama tunavyokulea wewe pamoja na uzima ovyo wako!”

    “Ahsante mama.” Henry alijibu haraka haraka na kuanza kuondoka huku akijifanya kama yale aliyokuwa akielezwa na mama yake yalikuwa habari za utani tu; lakini ukweli ilikuwa huko kichwani mwake tayari kulikuwa kumefumuka zogo fulani!

    Ndio, kile kichaa cha mapenzi juu ya Brigitte ambacho ingawaje ni kweli kilikuwa kimepungua sana, lakini hatahivyo, bado kilikuwa na uwezo wa kuendelea kumvuruga akili na hata kuweza kumfikisha katika kufanya maamuzi ya kipumbavu kwa hasara zake mwenyewe!

    Bado alihitaji ushauri nasaha!

    Ndio hili alifahamu vyema!



    “Mbona hunijibu?…Unadakia ahsante tu!” mama Henry aliuliza huku akitoa cheko jingine dogo ambalo dhahiri lilikuwa la kejeli; na alijua sana alimuudhi mwanawe kwa kumuuliza mambo ambayo hakuwa na ujasiri wa kuyatimiza. Hatahivyo, alifanya kumuuliza kama vile yalikuwa ni masihara ingawaje kwa namna fulani ilikuwa ni moja ya njia zake katika kumpatia somo mwanawe wa kiume wa pekee na kitinda mimba wake.

    Alikuwa mtoto wa sita.

    “Mama, sasa unaninyanyasa!” Henry alitunisha misuli hata tazama yake ilithibitisha.

    Ndio, alitupa jicho kali!

    Jicho la shari!

    “Nani akunyanyase? Wewe unafikiri ni nani atakayekuongoa kama sio sisi wazazi na nduguzo?” Mama Esta alijibu kimasihara, na kisha akafanya kama aliyekasirika na ndivyo aliingia kusema kwa ukali, “haya potea kabla sijakunyang’anya hela zangu!…ala!”

    Alijikuta akikimbiwa na hasira zake ambazo zilidhihiri zilikuwa ni kamasi!

    Alisinyaa pia akianza kujiondoa kinyongenyonge hadi mlangoni.

    Aliufungua mlango taratibu, kisha aligeuka na kumtazama mama yake kwa sekunde kadhaa…

    Hasira zikamrejea!

    Akafyonza na kutoka huku akiacha kaubamiza mlango wa jikoni kwa nguvu kiasi ulilia sana!

    Alitoka hadi uani.

    Huko alipitiliza hadi ilipokuwa imepaki gari yake aina ya landrover. Alizitoa funguo mfukoni mwake na kufungua mlango wa mbele wa gari.

    Tena akazichomoa funguo na kuingia garini; na kisha aliiweka simu yake ya mkononi ndani ya kichumba kidogo kilichokuwa wazi chini ya radio. Alishikashika kidogo usukani na kisha tena, akazichomeka funguo katika ‘switch’ kuiwasha gari.

    Alijaribu kwa safari kadhaa kuiwasha gari, lakini haikuweza kuwaka!

    Akajaribu tena na tena lakini wapi…

    Haikuwaka!

    Alitulia kidogo kama aliyekuwa akifikiria jambo fulani, halafu alibonyeza kitufe kimoja na kisha akatoka nje hadi mbele ya gari ulipo mlango wa chumba cha injini. Akaufungua mlango huo na kuanza kutazama ndani yake huku akijaribu kushika hiki na kile na kisha aliufunga tena mlango.

    Alishusha pumzi kidogo, akarejea katika mlango wa dereva, akasogeza mkono katika ‘switch’ na kuzichomoa funguo na kisha aliufunga mlango.

    Huku akisonya aliondoka zake.
    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Alirudi hadi chumbani, akaziweka funguo mezani na kisha alitoka.

    Alipofika uwani, akielekea lilipo geti la kutokea nje ya jengo, aliweza kuzisikia sauti za mama yake.

    “Hilo kopo si alitupe tu jalalani tujue moja!...Ooh, gari yangu, gari yangu! Wenye magari wasemeje?” Hizo zilikuwa sehemu za sauti hizo.

    Hapo hasira zilimzidia, na wala hazikuwa hasira dhidi ya mama yake; bali zilikuwa dhidi ya ule uhusiano wake na Brigitte jinsi ulivyopata kumpeleka hadi kumfikisha mahala ambapo leo hii amekuwa ‘mtu mzima ovyo huku kodi ya pango ni ubora wa shikamoo zake kwa hao wambebao!’

    Hasira hizo zilizokuwa sasa zimeibukia mawazoni kama mtawala mwenye mamlaka, mtawala mwenye madaraka; na zilikaribia kumfanya asitishe wazo la kwenda tabata. Ndio, tafsiri zenye ushawishi mkubwa zilimwandama na kumjulisha ilikuwa ni fedhea kubwa kwenda huko huku akijua kwa kufanya hivyo ilikuwa pia ni sawa na kumtembelea ‘mvurugaji’ aliyekuwa hadi wakati huo akiishi na Brigitte.

    ‘Marlon isn’t your friend, but an enemy within friendship! (Marlon ni adui katikati ya urafiki)’ Mawazo fulani yalimzaba kwa mwendo huu.



    Sauti za mama yake zilizidi kumvuta Henry hadi kujikuta akirejeshwa nyuma kimawazo kwa kukumbushwa habari za nukta chache kabla hajafikia uamuzi wa kukaribisha uundaji wa uhusiano wa kimapenzi na Brigitte. Tena hata alimkumbushwa jinsi rafiki zake walivyowahi kumuhasa juu ya hathari za kujenga uhusiano huo dhidi ya ujengaji wa bora za maisha yake ya usoni.







    Ndio, kumbukumbu ilimjia kwa kuitazama ile siku iliyounda uhusiano wao rasmi kule IFM.

    ‘Be very afraid lest you go down regrettably! (Ogopa sana usijute!)’ Sauti hii humtokea kila aikumbukapo siku hiyo ambayo kimsingi ndio ilizaa sumu iliyokuja kummaliza.

    ‘Rafiki, wewe ulisema!’ Henry aliijibu sauti ile moyoni huku akimkumbuka sana huyu rafiki yake ambaye alikuwa ndiye akimshauri sana aachane na mawazo ya kujiingiza katika uhusiano na Brigitte waliyemchukulia hakufaa kwa ushirikiano dhati wa mapenzi.

    Kwamba, rafiki zake walifananisha kumchukua Brigitte ilikuwa ni sawa na kujitumbukiza ndani ya lile shimo lililopata kuwepo kule Jerusalem hata kabla ya ujio wa Bwana Yesu; ni lile shimo lenye moto mkali uwakao daima, shimo ambalo Bwana Yesu alilifananisha na adhabu kali itakayotolewa siku ya Hukumu!

    Lile shimo liitwalo ‘Jehanamu’!

    Henry hakuzipatia nafasi shauri za jamaa zake licha ya yeye mwenyewe kuziona dalili, kwamba, Brigitte hasingemfaa kutokana na historia yake kujifunua kweupe katika kuwachukulia wanaume kwa mfano sawa na ATM!

    Hivyo, moto aliutaka mwenyewe!

    Huo kweli ulimchoma!

    Ukimbakisha mifupa mitupu huku Brigitte akiteleza mithili ya kamongo ndani ya tope la ziwa victoria!



    “Bwanae, sina mpango naye! Mimi nawatembelea watoto bwana! Kwanza, watoto hawagombewi!” Henry alijikuta akijisemea kwa sauti ndogo katika kuisuuza roho yake. Alikubali kujidanganya eti hakumtaka tena Brigitte, wakati ilikuwa ni ukweli usiopingika bado penzi lake kwa Brigitte lilikuwa na chachu kali tu ya kumuhitaji endapo lilitoneshwa. Ni Brigitte ndiye aliyekuwa hamtaki kwakuwa hakuwa na chochote tena cha kuvunwa kama ilivyokuwa huko awali!

    Hatahivyo, wakati mwingine Henry alikiri bado kumpenda Brigitte; lakini hivyo alikiri eti kwa kujiwekea sababu ilimpasa ampende kwakuwa alikuwa ni mama wa watoto zake!



    ****

    Henry alitembea kuelekea kituoni kwa kupiga hatua za taratibu. Na licha ya mwendo huo, bado safari haikuwa ndefu, kwani kimsingi kutoka nyumbani kwao hadi huko kituoni hakukuwa mbali.

    Ndivyo, ilimchukua si zaidi ya dakika kumi kuweza kufika kituo cha mabasi katika ‘soko la nyuki’ huko tegeta.

    Hakuangaza sana; kwani macho yake yalipoona basi moja dogo lililokuwa limeanza kujaa abiria, ndivyo aliamua kulifuata na kupanda.

    Baada ya watu kujaa, basi liliondoka.



    Baada ya dakika kumi hivi, basi lilifika kituo kimoja kidogo na kusimama. Hapo walishuka abiria wachache na kisha tena abiria wengine walipanda, tena basi lilianza kuondoka...

    Mara ilisikika sauti!

    Mwizi! Mwizi! Mwizi!

    Hizo zilikuwa ni kelele za mwanamke mmoja aliyekuwa katika moja ya viti vya katikati katika basi hilo na akiwa upande wa dirishani; na hapo tayari alikwishainuka.

    Dereva hakuongeza mwendo mara baada ya kusikia kelele hizo; kwani badala yake aliamua kupunguza mwendo huku akilijongeza basi pembeni mwa barabara na hata kulisimamisha.



    Kondakta aligeuka nyuma na kumtazama yule mwanamke, kisha akamsemesha, “mama ni aje?”

    Mwanamke yule alianza kutoka ndani ya basi huku tayari akitokwa na machozi. Akitweta sana alijibu, “vibaka wamenipokonya pochi1!…Ni walee! Haoo, wanakimbilia bondeni!”

    Mwanamke yule alipotoka ndani ya gari, alianza kuwakimbiza vijana wawili ambao mara baada ya kuvuka barabara walielekea bondeni.

    Vijana wale waliingia uchochoro mmoja uliokuwa katikati ya nyumba mbili mbovumbovu katika bonde hilo ambalo huko nyuma lilikuwa likitumika kuvuna mawe, kokoto na vifusi vya ujenzi. Hatahivyo, watu wachache kiasi walijitokeza kumsaidia kuwafukuza vijana wale huku kukiwa hakuna hata abiria mmoja aliyetoka kusaidia.

    Si kitambo kirefu tayari dereva aliondosha gari kumuacha mwanamke yule akitokomea bondeni.



    Baada ya dakika arobaini na tano hivi au zaidi kidogo, basi lilifika kituo cha kariakoo.

    Abiria kadhaa waliteremka akiwemo Henry.

    “Nadhani ni mgeni huyu mama!” Jamaa mmoja alimwambia Henry walipokuwa wameshuka.

    “Kwanini unasema hivyo?” Henry aliuliza kidaku.

    “Ni rahisi kumtoa mtu kijijini lakini ni vigumu sana kuutoa ukijiji kichwani mwake.” Jamaa yule alijibu.

    “Mshikaji umeniacha njia panda…ukijiji ni nini?” Mtu mwingine alidakia mazungumzo.

    “Kuutoa ushamba kichwani mwa mtu ni kazi ngumu, lakini…to take him out of the bush is not a big thing.” Mtu yule alifafanua ule msemo wake, kisha tena aliendelea, “She’s a bush woman with a bush in her head…Mjanja hachapwi mtindo huo!”.

    “Ugeni wa mtu si sababu, habari ni mtu kuwa chugachuga! Mademu wengi hupenda kunata sana kiasi hujikuta wakijiachia ovyo wakiona kila kitu ni rahisi rahisi.” mtu mwingine alidakia pia huku akimtazama zaidi mtu yule kwa kupeleka macho ya kusahihisha uelewa wake.

    Henry hakuchangia; badala yake, aliwaacha watu wale na kuanza kupiga hatua kuelekea maeneo ya ‘shule ya uhuru’ kilipo kituo cha mabasi yaendayo tabata-mawenzi.



    ****

    Kwa kuwa abiria walikuwa wengi, Henry aliamua kupanda basi la ‘tabata-segerea’ kutokana na kupata urahisi wa kupata nafasi ya kuingia.

    Muda kidogo safari ilianza…



    Baada ya kama nusu saa hivi, basi lilifika kituo cha ‘bima’ na kusimama kidogo kuruhusu abiria kadhaa kuteremka ikiwa ni pamoja na Henry; na abiria wengine kadhaa walipanda basi hilo kabla ya safari kuendelea tena.

    Henry alivuka barabara na kisha alianza kuifuata barabara ya mawenzi; lakini hakuifuata kwa umbali mkubwa kabla ya kuingia uchochoro mmoja. Alitembea hatua kadhaa, akaingia uchochoro mwingine, akapinda kona moja na kuingia tena uchochoro mwingine zaidi hadi alipoikamata barabara moja isiyokuwa na lami iliobatizwa jina la ‘Barabara ya Damascus’. Hiyo barabara ilikuwa ni mtaa wa tatu hivi kabla ya kuufikia ule mtaa aliokuwa akiishi kijana mmoja (Bob Jamex) aliyejulikana kwa ucheshi eneo lote la mawenzi.

    Henry alizivuka nyumba kama tano hivi hadi alipoifikia nyumba moja ya ghorofa moja iliyokuwa ikitazamana na duka moja. Hapo alisimama.

    Hiyo ilikuwa nyumba aliyokuwa akiishi Brigitte na Marlon, mpenzi wake wa wakati huo; ndio, pia ilikuwa ni nyumba ileile aliyopata kuishi yeye na Brigitte kabla ya kufarakana kwao.

    “Shikamoo bro!” Alisema kwa sauti kubwa, kijana muuzaji wa duka lile aliyekuwa ameketi nje ya duka katika benchi la kukalia wateja.

    Henry aliitikia kwa kupunga mkono wa kulia, na kisha alizipanda ngazi hadi juu ghorofani ambako ndiko waliishi wakina Brigitte. Kisha tena alianza kuufuata mlango wa kuingilia ndani; alipoufikia, aliinua mkono wake wa kushoto hadi kilipokuwa kitufe cha kubonyezea kengele, na kubonyeza mara mbili tatu hivi kabla ya kukiacha.



    Mlango ulifunguliwa baada ya kitambo kifupi, na mfunguaji akiwa Brigitte mwenyewe.

    Kwanza, walitazamana bila sauti kuwatoka; ni kwamba, wakati mmoja kati yao alitazama kwa kutumbua macho huku mwingine akitazama mithili aliyekuwa akiangalia kitu fulani cha kawaida sana na kisicho na uzito kushtusha mtu.

    Hatahivyo, kidogo tena Brigitte alilibadilisha tazamo lake, kwani hali za huruma zilimvaa kidogo na hivyo kuwa sehemu ya shuhuda kwamba wakati fulani hata jambazi hupatwa na huruma ijapokuwa kwa asilimia nyingi sana huruma yake huwa ni ya kiwango kidogo na ya muda mfupi sana!

    Ndani ya hisia zake, Henry alikubali bado ‘alimezwa’ kimapenzi! Ndio, alikubali alimezwa, kwani hata mawazoni alinena kudhihirisha ukubali huo, ‘hakika, itanichukua muda mrefu kuweza kukipatia tiba halisi hiki kidonda cha penzi!’



    II



    Hapo mlangoni, Brigitte Mingly alivalia kaptula fupi sana kiasi iliweza kuruhusu macho yoyote ambayo yangekuwepo hapo kushuhudia uzuri wa mapaja na miguu yake, kwani kwa hakika Muumbaji aliifanya kazi yake barabara!

    Kama ni mapaja, hayo yalifanana kama sio kuwa jirani sana na yale ya muimbaji maarufu wa kimarekani (Jennifa Lopez); nadhani hata naye ingekuwa ni ‘swadaktan’ kama angeyakatia bima!

    Kama ni miguu, hiyo ilikuwa ‘bia hasa’ mithili ya Tina Turner asiyezeeka!

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Oho…mambo! Karibu ndani!”

    Ni hiyo sauti nyororo iliyomshtua Henry na kumrudisha tena katika hali yake ya kawaida.

    Ingawaje Henry aliupokea vyema ukaribisho huo na hivyo kuonesha kufurahishwa sana, lakini ndani ya mawazo yake alitengeneza tafsiri mbili; mosi, huo aliuchukua vyema, na pili, huo aliuchukua sawa na tabasamu la mamba ukidhania hawezi kudhuru!

    “Ahsante.” Henry alijibu huku akiingia ndani.



    Brigitte alijua Henry alikuwa bado mbabaikaji. Hivyo, alichekelea moyoni ‘meli’ (Henry) ilikuwa ndani ya himaya yake ingawaje ni bahati mbaya ilikuwa bado haijapakia mizigo mingine. Hilo bila shaka ndilo alikuwa akisubiri kwa hamu litokee ili atumie nafasi nyingine ya kuwa mpakuaji.

    ‘Kwanini isitie nanga hapa?’ Alijiuliza Brigitte wakati akimsaili kiaina; na wakati huo, Henry aliketi sofa la pembeni. Lakini hakuruhusu kuwaza zaidi, baada ya kumuibukia na swali lililobebwa na sauti laini ya kirafiki, “Sijui nikuletee kinywaji gani babaa?”

    “Bia yoyote itafaa…lakini sio 'the kick'.”

    “You don’t like going kicky?”

    “Umepotea…huko sipatikani!” Henry alijibu kimasihara huku akicheka, kwani alijua Brigitte alimjua fika bado hakuwa mtu wa kunywa ‘ngoma nzito’.



    Brigitte alichomoka hadi kwenye jokofu, akatoa chupa ya bia aina ya ndovu na kurejea nayo.

    “Sikosei unapendelea baridi.”

    “Hapo umeniita vyema!” Henry alitania tena.

    Brigitte aliiweka bia katika kijimeza kidogo kilichokuwa pembeni ya sofa. Alienda kabatini na kuchukua glasi; na kisha, aliileta katika meza ile.

    Alifungua kizibo cha bia na ndipo Henry alikaribishwa, “karibu baba watoto.”

    Mazungumzo ya kawaida yalianza.



    Muda uliposonga sana huku Henry akiwa haoni dalili za kuletewa watoto, ndipo aliamua kuuliza kwani hilo ndilo hasa lilifanya aje hapo.

    “Samahani. Ni kweli hawapo. Nimewahamishia morogoro kwa mama yao mdogo. Watasomea hukohuko.” Brigitte alijibu kwa utaratibu utadhani alikuwa ni aina za wanawake wanyenyekevu.

    “Sawa, ila ingenoga sana kama tungeshauriana kwanza...Au kwakuwa...Aah, wakati mwingine wanishangaza sana!”

    Brigitte hakujibu; taratibu alianza kujiumauma!

    “Anyway, yaishe.” Henry aliamua kuutokomeza mjadala, maana aliona dalili za hali ya hewa kuelekea asipopenda zielekee. Alimuelewa sana Brigitte.

    Brigitte alimtazama Henry kwa muda huku akiumauma meno yake, lakini ghafla alijikuta akiangua kicheko kifupi. Hilo lilikuwa ‘cheko-sanifu’!

    Aliinuka alipokuwa ameketi na kuongoza hadi katika jokofu; na aliporejea, alikuwa akinywa kinywaji aina ya Heinken katika kopo.



    Kimya kilitanda kama dakika tano hivi au zaidi kidogo hadi pale Henry alipoamua kuaga. Alikuwa kishamaliza bia yake, “sasa nakukimbia. Unajua kuna sehemu nataka...ahm, nawahi sehemu. ”

    Ndio, Henry hakuona tena umuhimu wa kuendelea kuwapo pale, kwani aliowafuata hawakuwepo; na pia aliona kuendelea kutazamana na Brigitte kulikuwa ni sawa na kujikumbusha maumivu ambayo alikuwa akijaribu kuyasahau.

    “Kwakuwa watoto wako hawapo ndio unaaga mapema namna hii! Sio fresh mzee!” Brigitte alisema kinyonge ingawaje uso wake haukuuzungumza unyonge halisi.

    “Nilikuja kwa ajili yenu wote, ila ni kweli nawahi sehemu…please, understand!”

    “Acha hizo…kaa kidogo babaa!” Kabla ya Henry hajajibu, sauti hiyo yenye uwezo wa kumtoa nyoka pangoni iliendelea kusema kwa namna kwamba mjadala ulifungwa tayari, “vipi, tuongeze?”

    “Skiliza Jose…?”

    “Babaa…kama hutajali, kuna gari itakuja kunichukua. Unaonaje usubiri kidogo babaa? Nitakusogeza mbele. ” Brigitte alikatiza huku akiinuka ili kufuata chupa ingine ya pombe.







    “Sawa.” Henry alijikuta akijibu.

    Aliletewa pombe ingine.

    “5” Haikupita muda sana, Mara Marlon Evans aliingia.

    “Habari yako.” Alimsalimia Henry na kwenda kukaa kwenye sofa kubwa alilokuwa ameketi Brigitte Wingly.



    Tangu Marlon afike, Brigitte alianza kubadilika na kuonyesha kila dalili za kujawa na hasira, kwani Henry alishuhudia hata hawakusalimiana!

    Hii ilimrahisishia Henry kuweza kuufukuza wivu wake (ulionyauka) uliomjia baada ya kufanywa mtazamaji kwa kuwaona Marlon na Brigitte wameketi sofa moja wamekaribiana sana.

    ‘Bado umependa, bado umeoza!’ Sauti moja iliyojitengeneza mawazoni mwake ilimsemesha Henry kabla hajafanikiwa kuahirisha maumivu ya wivu huo kwa kuingiza dharau.



    Kimya kilitanda hadi pale sauti ya honi ya gari iliposikika huko nje.

    Brigitte hakugutuka sana kwa habari ya mlio wa honi ile, isipokuwa alitulia kidogo na kuwa kama mtu aliyekuwa akitafakari. Baadaye, mara aliyaachia wazi meno yake meupe yaliyochongoka vizuri huku uso wake ukijilembesha taaswira ya mtu mwenye amani, mtu mwenye furaha, mtu mwenye kujiamini.

    Marlon akatazamwa;

    Kwa macho ya mahaba alitupiwa!

    Kwa macho ya kupendwa alitazamwa!

    Kwa macho ya kitandani alikodolewa!



    Hapo Henry alishangaa kidogo kabla ya mawazo yake kuanza kuujadili ujio huo wa ghafla wa tabasamu la Brigitte; pia wivu ulimpasua kidogo kwa kule kuona mwenzake akitupiwa lile tazamo ambalo alikumbuka alikuwa ‘akiwashwa’ sana kila lilipozaliwa kwa ajili yake! Ndio, kiasi, hisia zake zilimkumbusha utamu wa kutazamwa vile ambavyo sasa ni mwingine alikuwa mzawadiwa!

    Ujadili huo uliibuka na neno ‘hapana’, kwamba, hivyo uliibuka ukikataa haikuwa kweli tabasamu la Brigitte liliwasilishwa hapo ndani ya njema za dhati!

    Ndio, ujadili ulikataa!

    Kwamba, hapo ujadili uliitikia hilo lilikuwa ni tabasamu lililoficha dhamira fulani iliyoelekea kunuka sana; kwamba, hilo lilikuwa ni janja ya Brigitte kufanikisha kutumbukiza udanganyi ili iliyofichwa isifichuke!



    “Marlon, tunatoka na Baba Johan.”

    Ebo!

    Henry aliitika huku mjadala ule ukilazimishwa sasa kukatika mawazoni kwasababu kuitwa kwa jina hilo kulimshangaza sana!

    Ndio, Henry alishangaa sana, kwani ni miaka mingi hakuwahi kusikia mdomo wa mzazi mwenziwe ukimuita jina hilo!

    Ndivyo, ilikuwa taratibu alijikuta akisogezwa, na akikenua meno yake…

    Kwamba, faraja fulani ilimjia!

    Akifurahi kuburuzwa na ujinga wa hisia!



    Ndio, Henry alifurahi kijingajinga kusikia akiitwa ‘Baba Johan!’ Lakini furaha hiyo haikuweza kusafiri zaidi ya sekunde kumi hivi, kwani ilikuja kukatizwa kwa kishindo cha ghafla pale alipojikuta akichotwa na wivu uliomjia tena mara baada ya macho yake kushuhudia Marlon akisogelewa karibu zaidi huku akishikwa mkono…

    Isitoshe, akashuhudia zaidi…huyo akipigwa busu, akipigwa busu murua la shavu ambalo dhahiri aliona jinsi lilivyomtetemesha Marlon!

    Hapo hali ikabadilika, kwani pumzi zilishuka chini kwa kasi kiasi alikuja kupata shida kuzivuta zingine kutokana na hali ya kujihisi ovyoovyo kumnyakua mithili ya kifaranga cha kuku dhidi ya makucha makali ya mwewe yaliyoshikilia imara!

    “Uuh!” Sauti ilimtoka; lakini hatahivyo, alipogundua aliweza kuituliza isitoke tena huku akibakia akijiumauma. Na tayari sauti moja katika mawazo yake ilimsemesha, ‘tulisema bado umependa, bado umeoza…bisha!’

    Brigitte hakuyaona mabadiliko ya Henry, kwani akili na mawazo yake yote vilihamia kwa huyo mpenzi wake ili kuhakikisha akifaulu kumlainisha.

    “Sweetie, nimeitwa kwa mambo ya watoto. Hivyo huenda nikachelewa kurudi.” Brigitte alisema kimsisitizo huku akikazana kuvichezea vidole vya Marlon.

    Brigitte hakusubiri kujibiwa; aliinuka taratibu, akampiga busu moja katika paji lake la uso na kisha alisema kwa mwendo kama vile tayari walikubaliana, “leo ulale honey ili uchunge usalama wa nyumba.”

    Marlon alipepesa macho bila kujibu kabla ya kujikuta akiyagandisha kwa kumtazama Brigitte pale alipoanza kuondoka.

    Ndio, Brigitte aliondoka huku akihakikisha ‘mitetemeko ya nyuma’ ikizidi kutawala mawazo ya Marlon; na huko mawazoni msemo mmoja ulimkumbusha ‘mwili wa mwanamke ni kujua kutawala mawazo ya mwanaume!’

    Kidogo, Marlon naye aliinuka, akaanza kumfuata Brigitte huku Henry akibakishwa mtazamaji…



    Mawazo ya Henry yalipotulia, aliinuka na kusogea dirishani ili kuchungulia kama hiyo honi ya gari waliyosikia ilikuwa ndio ile gari aliyosema ingekuja kumpitia.

    ‘Must be the one!’ Aliwaza baada ya kuiona gari. Kisha alirudi na kuketi huku sasa akianza kuhisi Brigitte alikuwa ameanza kucheza ‘mpira mchafu’; kwamba, hisia zake zilinena uhusiano wa wawili hawa ulikuwa tayari ukielekea kuanza kumeguka ukiachia ‘mushkeli maeneo fulani’ kujiibua nje ili hatimaye kweli watibuane!

    ‘Ina maana siku hizi halali hapa?’ Henry aliwaza zaidi; na ndivyo wivu wake ukaanza kumkimbia tena katika kumuacha akiwa muwazaji wa atazamayo.



    Baada ya dakika kumi hivi Brigitte alitoka chumbani huku akiwa kavalia mavazi mengine, mavazi ya usiku.

    Marlon hakuonekana!

    Hakutoka!



    ‘Sijui jamaa ananiwazaje? Labda afikiri mzee wa kiwanja nimerudi katika himaya!’ Aliwaza Henry.

    “Baba Johan, twende zetu. Achana nalo!” Brigitte alisema kwa sauti ya chini wakati wakiwa tayari mlangoni.

    ‘Hisia zangu ni sahihi…hapa mchezo umeanza!’

    Walitoka nje, na kuingia garini huku Brigitte akiketi kiti cha mbele.



    “Mshikaji, unafikiri! Jamaa lachungulia dirishani!” Brigitte alimueleza dereva kabla ya kuangua kicheko cha kebehi ambacho kiliongezwa nguvu na kile cha dereva kilichofuatia. Wawili hao walionekana kufahamiana sana.

    “Kukandamiza ni uzito wa mkandamizaji…kama uzito umekwisha, wewe ni kuanza tu sister!” Dereva alidhihaki huku akiirekebisha radio ya gari.

    “Hakuna ponyoo…” Brigitte alisema na kuachia usemi wake kama vile alihitaji mwingine amalizie.

    “Hakuna kupenyee!” Dereva akamalizia.

    Wakacheka tena.



    “Mshikaji, huyu hapa ndiye mume wangu, lakini hana kokolo wala gozigozi…..Hilo jamaa ni jizi kama hili jizi jingine tunalolifuata huko De-paradise.” Aliendelea kusema Brigitte mara baada ya vicheko vyao kusimama.

    Henry alisikia kichefuchefu!

    “Mijitu mingine bwana, yaani hawajui siku hizi hakuna mapenzi bila ATM…ndio, pesa kwisha mapenzi kwisha vilevile! Pochi likikoma, mwanamke ni kudandia daladala nyingine kwa kasi mpya na ari mpya…ala, mjini shule ati!”

    Yule dereva aligeuka nyuma na kumtazama Henry, kisha alikenua meno yake yaliyoungua huku akimwaga tabasamu lake lililoficha kidogo tafsiri ya kusikitika; kisha aliirudisha tena shingo yake mahala pake ili kuendelea kumakinisha akili katika uendeshaji. Sasa hakucheka; na wala hakutia neno. Ni kama vile alichotwa mawazoni.

    ‘Mmh! Yaani, nadharirishwa kiasi hiki mbele ya mwanaume mwenzangu…Ana akili kweli huyu?’’ Henry aliwaza huku hasira zikimjia; na ndivyo hata alianza kujuta ni kwanini aliamua kuja huku!

    ‘Bado nafanywa bwege waziwazi?’

    Henry alitamani kushuka, lakini wazo jingine lilimkataza kufanya hivyo.

    Upumbavu wake ulimkataza!

    Upumbavu?

    Ndio, ule upumbavu wake ulipata nafasi nyingine ya kutawala mawazo yake na hivyo kuzaa upumbavu mwingine - Eti aliona ilikuwa ni jambo la busara kutoshuka na wala kutoonyesha kuchukizwa na yote hayo ili aweze hatimaye kurudi tabata peke yake ili kumsaidia Marlon kwa kumuelezea ukweli wa wapi Brigitte alipokuwa amekwenda!

    Na isitoshe eti aliona ilikuwa ni vizuri amsaidie katika kupanga mikakati ya kumuadabisha Brigitte!

    Kumuadabisha Brigitte na ili iwe nini?

    Eti kusaidia penzi lao liimarike, lisibomoke!

    Yaani, amlinde mwizi wake aendelee kumuibia; kwamba, amsaidie huyo kuimarisha uvunjaji wa ndoa yake? Au ni kwakuwa alibwaga manyanga?

    Ndio, hivyo eti aliona ulikuwa ufumbuzi muafaka mbele za fikira zake ili kumsaidia Marlon!

    Hivyo ndivyo bunge la mawazo yake lilivyojadili sakata hilo hadi kufikia maamuzi hayo, tena kwa mwendo wa ‘kura zote za ndio’!

    Tena eti, kwa kuyafanya hayo maamuzi ilikuwa ni sehemu ya kulipa fadhila za kulelewa watoto!

    Yote hayo yalikuwa ni vizaliwa vya ‘utegemezi’ ambao kwa hakika ni kichaa kibaya sana ambacho kinapokosa ‘pendo lake’ huweza hata kumfanya mtu ajikute akifikia hatua ya kutenda uovu kama vile kujiua au kufanya matukio ya kinyama kwa jamii husika na isiyo husika!

    Ni kwamba, Henry alizidiwa maarifa na upumbavu huu mwingine uliokuwa umeyeyusha yale machungu yake yaliyoletwa na ule utegemezi; na ndivyo haikuweza kabisa kumuingia akilini kuwa ni Marlon ndiye aliyewasababishia watoto wake wakose malezi ya baba na mama, na hivyo kuwapelekea katika maumivu makali ya kiakili. Henry hakupata kufikiria kwa kiwango gani huyu Marlon na wale wengineo walikuwa ndio waliomvurugia utaratibu wa maisha yake akiwa na Brigitte kama mkewe!

    Ndivyo upumbavu ukamgawia rungu imara la kuendelea kuvuruga mambo na kujivuruga pia!



    Wakati Henry akivamiwa na upumbavu huyo, Brigitte aliendelea kuzungumza na dereva wake kwa vicheko vya hapa na pale bila kun’gamua chuki kali ya Henry dhidi ya hali nzima iliyokuwemo ndani ya gari hilo!

    Brigitte hakujua tayari Henry alikuwa mwenye hasira kali yenye kumtengenezea sumu ambayo ilikuwa ni lazima itapikwe!



    Walipokaribia kituo cha basi cha mwenge, Brigitte aligeuza shingo yake na kutazamana na Henry, kisha alisema, “tukushushe mwenge au unasemaje?”

    “Ahm…ok. Ahsanteni!” Henry alijibu kwa kujitahidi kuchangamka.

    “Hey, gone full of you? (Una mawazo sana?)” Brigitte aliuliza kidadisi.

    “Aah…ahm, hapana!” Henry alishindwa kujibu vizuri huku akiingia harakaharaka katika kufikiri.

    “You look disconcerted! (Hujatulia!)”

    “It’s…ooh, ni tumbo! Lanisumbua sana! Aah, ni tangu jana lilianza!” Henry alifanikiwa kudanganya.

    Baada ya Brigitte kutoa pole yake, pia dereva aligeuka na kuisema pole yake huku mdomo wake ukielekea kama vile ulitamani sana hujiruhusu ucheke.

    Henry aliona yote.

    “Nitakwenda kujisaidia katika choo cha hoteli pale kituoni…ondoa wasiwasi.” Henry alijibu.



    Walipofika mwenge, Obrien alilipaki gari pembeni mwa barabara na hapo Henry akafungua mlango na kutoka nje.

    “Samahani babaa! Ebu njoo huku.” Brigitte aliita.

    Henry aliitikia wito, akasogea hadi dirishani. Akasimama hapo kwa kukiinamisha kichwa chake.

    “Najua mshikaji!…hatahivyo, usikonde sana. Kamata hawa wekundu wawili wa msimbazi ili kuchangia kusukuma gurudumu lako la maisha, au vipi my my?” Brigitte alitoa noti mbili za shilingi alfu kumi na kisha akampatia Henry.

    Henry alitaka kukataa kuzipokea lakini alishindwa kufanya hivyo, na hakujua ilikuwa ni kwa nini iwe hivyo hata alishindwa! Ila sababu za kutaka kuzikataa ilikuwa ni kule kutopendezewa na jinsi Brigitte alivyompatia huku akibibitua midomo yake kwa kejeli; naam, hali hiyo ilimfanya aone tukio hilo kama udharirishaji!

    Lakini…

    Lakini, pengine alikubali kuzipokea kwakuwa ‘alipauka sana’ ashindwe kusimamisha ujasiri wa kuzikataa!



    ***

    Kwa kuwa ule upumbavu ulikuwa umemganda sana, basi ndivyo Henry aliingia kituoni hapo kwa kutanguliza laghai eti alikuwa akienda kwanza msalani kupunguza maumivu ya tumbo lile!

    “Hivi utakua lini Brigitte?” Alijisemea kwa sauti ya chini huku akiongoza njia kuelekea yalipokuwa mabasi ya tabata mara alipoingia ndani ya kituo huku akiwa na uhakika hakuonekana sasa.

    Safari hii alipata basi la moja kwa moja hadi kituo cha kimanga-mawenzi.



    Ilimchukua kama dakika 45 hivi kufika kituo cha kimanga-mawenzi ambako alishuka na kuanza kutembea taratibu akiingia barabara ya mtaa wa Damascus.

    Alipofika mbele ya nyumba ya Brigitte, alisimama na kupigapiga viatu vyake kidogo…kisha, taratibu alianza kuzipanda ngazi huku mawazoni akijiuliza sana kuhusu ni kwa mwendo upi Marlon ‘angelipuka’ baada ya kuelezwa ukweli wa mambo!





    ****

    Asubuhi ya saa moja na nusu katika siku ya tarehe 21/08/1989 ilimkuta John Hughes akiwa mezani akipata kifungua kinywa kilichokwenda kwa chai ya kahawa pamoja na mkate uliokaangwa kwa kuchanganywa na mayai; na pembeni yake, suria aliyekuja baada ya kumuita alikuwa amechuchumaa kwa heshima.

    “Dadaako amekuonyesha nguo nilizokuletea jana?”

    “Ndio, nashukuru sana shemeji.” Msichana huyo aliyeitwa Jackline alijibu kwa kuachia sauti ndogo huku uso wake ukiachanua tabasamu.

    “Zimekukaa safi?” Hughes alisema huku mkono wake mmoja ukimshikashika kichwani kwa kufanya kuzilaza nywele zake ambazo hatahivyo zilikuwa zimelala vyema.

    Jackline aliitikia kwa kichwa akimtazama Hughes kwa macho ya aibu huku akiziumauma kucha zake!

    “Amekupatia?”

    “Ndio, alinipa jana hiyohiyo. Nashukuru.”

    Akimpiga kofi la masihara, Hughes alisema tena baada ya kupiga fundo moja la chai, “yote ni kwasababu napenda nikuone unapendeza.”

    Jackline alishukuru kupitia sauti ileile ya aibu huku bado akiuma meno yake; pia kichwa chake kilijilaza upande kidogo na hivyo kuonyesha ishara za unyonge, ishara za kukunika kindanindani.

    Mkono wa Hughes uliteremka kidogo katika paji la uso wake wa mviringo, kisha alimsemesha tena, “napenda kwasababu natamani mchumba akuone unavutia.”

    Jackline alijitahidi kujibu huku mdomo ukiendelea kumchezacheza; na pia alijaribu kuusogeza uso wake mbali kidogo dhidi ya mkono wa Hughes uliokuwa bado ukimvuta kiaina, “Shemeji sina mchumba! Halafu…aah! Kwanza mi bado mdogo…sipaswi, miye mdogo!”

    “Najua huna. Ila namzungumzia yule mpenzi aliyepo mawazoni kama ulivyomchora huku ukiwa pia umempachika sifa fulani.”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kaka wewe…aay!” Jackline alijibu huku bado akijitahidi kusogeza kichwa chake mbali kwakuwa hakupenda vile alivyokuwa akishikwashikwa. Lakini si kwamba hakupenda kushikwa vile kwasababu za kumuhisi vibaya Hughes, la hasha, hakumuhisi vibaya hata chembe; isipokuwa, aliona haikuwa vyema kuruhusu kushikwashikwa huku akiwa hajui angejiteteaje endapo angeambiwa ajieleze ni kwanini hakupenda kushikwa vile na mtu aliyefikiri hakuwa na dhamira chafu!

    Ni vibaya tu, yeye aliona huku akiwa asiyechukia kushikwa vile kwasababu alijua aliyemshika alikuwa ni shemeji yake ambaye hakutaraji angeweza kuwa na nia ya kutaka kumchota kwa hila ili hatimaye awe ndiye mfundishaji katika kumdondosha; ndio, alichojua ni kwamba, shemeji yake alikuwa mpenda masihara ambaye alimjali sana kiasi hata moyoni alirudia usemi huku akitazama chini kwa macho ya aibu!

    “Ebu nitazame nifurahi!” Alitania Hughes huku akijaribu kuuvuta uso wake kwa kumshika shingoni.

    “Shemeji!” Jackline alisema huku akikaza kichwa chake kisiweze kusogea ingawaje aliishia kujikuta akiruhusu kisogezwe…aibu ilimdaka hasa; lakini bado hakuhisi kuwepo kwa ubaya wowote, kwani uelewa wake ulikomaa katika kuona shemeji yake alifanya masihara kama ilivyokuwa desturi zake!

    Lakini pia hakuwa akipenda kutazamana na shemeji yake ili kuona ulegelege wa macho yake ambayo alikubali yalikuwa mazuri yenye mvuto maridhawa; ndio, tuseme huko moyoni tafsiri ilinena katika kukubali kwamba Hughes alikuwa na macho mazuri ambayo angetamani kila wakati awe akiyatazama huku yeye pia akitazamwa na macho hayohayo, kwani halikadhalika alikubali ilikuwepo raha iliyokuwa ikimmendea kila alipofanywa kutazamana!

    “Macho yako yanavutia!” Hughes alimtania tena mara baada ya kufanikisha kumfanya watazamane ijapokuwa ilikwenda kwa sekunde moja tu, kwani mara moja Jackline aliacha kumtazama kwa kupeleka tazamo chini huku akichekacheka.

    “He! He! Hi! Hi!”



    ****

    Katika umri wa miaka 48, tayari John Hughes alikuwa ni askari mzoefu wa karibu miaka thelathini huku akiwa ametimiza miaka mitano toka apandishwe cheo kuwa inspekta; pia, huu ulikuwa ni mwaka wake wa ishirini na tano tangu kufunga pingu za maisha na mkewe Lana Job.

    Kupitia mpango wa uzazi, walibahatika kupata watoto wawili wa kike, waitwao Doris na Dorin; watoto hawa waliishi nchini Uingereza huku mkubwa tayari akiishi maisha ya kujitegemea. Lakini, Dorin aliyekuwa mdogo alikuwa bado akisoma.

    Baba Doris au John Hughes alikuwa mweupe kiasi, mwenye pua iliyochongoka kidogo huku ‘lips’ zake zikiwa zimejaa. Macho yake makubwa na malegevu kiasi yalifanya awe katika muonekano ambao uliweza kuendesha ‘puta’ idadi kubwa ya wanawake; na hili lilimsaidia sana, kwani upande mwingine ni kweli alikuwa mlafi wa ngono akitamani kutembea na kila mwanamke jicho lake lilipopata kumtamani.

    A boozy womanizer!

    Hakuwa na uso mpana, ingawaje haukuwa wenye kuweza kuitwa mrefu; na huo ulibeba nywele nene na nyeusi sana (kipilipili) zilizokuwa daima zimepunguzwa. Isitoshe, kama angeamua kuziachia ndevu zake, ni hakika hizo zingekuwa nyingi zilizoshindiliana.

    Alikuwa na urefu wa kawaida huku mwili wake ukiwa mpana kiasi kutokana na kuwa na kifua kikubwa huku kitambi kikiwa kimeruhusiwa kujijenga kiasi.



    Hadi wakati huo John Hughes alikuwa akiishi na mkewe, wakiishi na mama mkwe pamoja na mfanyakazi wa ndani aitwaye Jackline. Hatahivyo, yapata zaidi ya mwaka mmoja tangu waanze kuishi na mama mkwe ambaye alikuja na mfanyakazi huyo baada ya yule wa awali (Shabana) kuamua kuacha kazi ili kwenda kuishi na mchumba wake huko manzese kwa mfuga-mbwa.



    Alijuana na Lana Job Jijini Mwanza ambako alipelekwa kwa ajili ya ‘kazi maalumu’; ndio, wawili hao walikutana kwa mara ya kwanza baada ya mazingira kuwakutanisha kwa kuwafanya kuwa abiria katika taxi moja ambayo Lana alizoea kuipanda.

    Hiyo siku ilikuwa jioni ya ijumaa yenye ubaridi mchanga uliozidishwa kiasi na uwepo wa upepo mwanana uliokuwa ukipiga kutokea ziwa nyanza.



    Lana alikuwa ndani ya taxi hiyo wakati iliposimamishwa na Hughes aliyekuwa kasimama nje ya jengo la Mwanza Hotel mara baada ya kuiona kibahati wakati alipotoka kutafuta usafiri wa kumzungusha mjini kutokana na kuchoka kukaa hotelini hapo ambapo alifikia kwa mwendo wa ‘kazi maalumu’.

    “Dada, samahani! Naomba nizungumze na huyu jamaa, kwani ametokea kuwa mteja mzuri sana.” Dereva alimueleza Lana aliyekuwa ameketi nyuma.

    “Ok.” Lana alijibu huku akisogea taratibu dirishani, kwani tayari alijikuta akivutwa kumtazama Hughes ambaye alikuwa bado akiashiria gari lisimame. Alishusha miwani yake myeusi chini kidogo, na kuanza kutazama.

    “Jamaa ni mgeni.”

    “Mmh, ok! Ok!” Lana aliitikia.



    Gari hiyo ndogo aina ya Nissan ilisimama mara ilipomfikia Hughes aliyesimama kando ya barabara; na ndipo yeye pia alisogea dirisha la mbele la mlango wa upande wa abiria huku tayari wakirudishiana salamu na dereva. Alipofika dirishani alitupa jicho moja la harakaharaka ambalo lilimjulisha abiria alikuwa mwanamke, na kisha aliliondoa. Hakuchukua zaidi ya sekunde tano, ndipo aligeuza kichwa chake chote na kumtazama tena huku akimsalimia, “salama bibie?”

    “Salama tu kaka.” Lana Job alijibu taratibu.

    ‘Mvuto hata katika sauti!’ Hughes alijisemea moyoni huku akigeuza kichwa na kurejea kutazamana na dereva.

    Hughes alijua Lana (alikwisharejea kuivaa miwani) alikuwa akimtalii huku yeye pia akifanya kwa chati ingawaje si kwamba alifanya hivyo ndani ya zile hila zake; isipokuwa, hivyo alifanya kwakuwa kutazama uzuri wa mwanamke ilikuwa ni miongoni mwa raha zake!

    “Nilikuwa nasaka gari.” Hughes alianza kumsemesha dereva, “unajua sijachukua namba za simu yako, vinginevyo ningekupigia uje kunichukua…sasa naona…?”

    “Eeh, dada! Waniruhusu nimchukue Bro? Lakini kwanza nakupeleka wewe!” Dereva alimkatiza Hughes huku akigeuka kumtazama Lana na kufanya hata Hughes kugeuza kichwa chake na kumtazama pia. Yaani, kama ambavyo dereva alivyoachia tazamo lake kwa Lana, ndivyo hivyohivyo Hughes pia alibadilisha tazama zake na kumfanya kuonekana mithili ya mtu aliyekuwa akihitaji kuhurumiwa; na ndivyo Lana alijikuta akiachia mwanya wake akifanya tabasamu jepesi.

    “Ni mteja safi, usihofu.” Dereva aliongezea kusema.

    “Sawa.” Lana alijibu kwa sauti ya chini.

    “Ahsante sana!” Hughes alikurupuka kujibu kwa furaha huku akianza kufungua mlango aingie ndani.



    Ndivyo wakati fulani wakiwa ndani ya gari hilo katika ijumaa hiyo, macho ya Hughes hayakuacha kuangalia katika kioo cha mbele na hivyo kuweza kumtazama vizuri Lana; lakini baadaye aliacha kabisa kutazama katika kioo ili kuacha nafasi kwa yeye kutazamwa pia kwani ishara za Lana kushikwashikwa na aibu alikuja kuzibaini.

    ‘What a real hit she is!’ Hughes alipata kujisemea huku tayari akijifanya kuangalia mbele na wakati huohuo mkono wake mmoja ukichezea mashavu yake; yaani, hapo tayari alihisi akihitaji kumnasa!



    Walipoanza kuishika barabara ya balewa, dereva alisema na hivyo kuwa mfukuzaji wa ukimya uliowafunika kwa muda mfupi, “Bwana Mnoge. Sasa karibu tunafika kwa dadaangu. Dakika kumi na tano hivi zimesalia.”

    Hughes alifanya kama mwenye kushtuka hivi; aligeuza shingo yake na kumtazama Lana kwa kuachia zile tazama zake, na kisha alisema, “sasa dada…hatujuani unajua! Lakini…mmh! Kwani sidhani kama ni vibaya tukijuana japo kwa kujuana kwa kuanzia majina yetu.”

    “Ni uungwana kufanya hivi, au wasemaje dada hapo?” Hughes alisema zaidi katika kuongezea, na kisha ndipo aligeuka tena na kuanza kumtazama katika kioo kwa waziwazi huku akiachia tabasamu za midomo yake zijibainishe.

    Lana hakujibu!

    Naam, aibu ilimkamata huku hisia zingine zikiingia kumueleza haikuwa vyema kuruhusu Hughes kuwa ndani ya gari kwa staili hiyo; na ndivyo kila macho ya Hughes yaliposukumwa kutazama kwa njia ile ya kioo, ndivyo pia alijikuta akijitahidi akutwe kainamisha kichwa ili kukwepa macho yao yasiweze kukamatana.

    Ndivyo alishindwa kujibu huku akihisi mwili kutekenywa na kisichoonekana!

    Kiasi akitetemeka!

    Kiasi akisisimka!

    Kiasi akitokota!



    “Naitwa Mr Mnoge.” Hughes alianza kujieleza kwa kutumia jina hili la uongo ambalo ndilo hasa alitakiwa kutumia wakati wote akiwa jiji hilo kwa ‘kazi maalumu’.

    Aliamua kuanza kujieleza ingawaje kiasi fulani aliziona ishara za Lana kutopendelea wasogeleane; lakini hatahivyo, kwa kuzijua tabia za wanawake za kupenda wachokonolewe zaidi kabla ya kujiruhusu kulegeza dhibiti zao, ndivyo aliona ilikuwa ni muafaka yeye kujipeleka kwa kujisogeza hivyo huku akiziunda ishara na shawishi za kimwili katika kusaidia kumvuta.

    Aligeuza tena kichwa chake ili kumtazama Lana kidhahiri; na kwa uzoefu wake alijua tayari alianza kufanikiwa kumlendemsha kabla hajaamua kama aanzishe rasmi vita vya kumtungua.





    Moyoni alicheka sana!

    “Mwenzangu waitwani?”

    Dereva alikuwa akitabasamu, kwani kwa siku chache tu alizopata kumpatia huduma Hughes tayari alianza kuufahamu ulafi wake kwa wanawake.

    Safari hii Lana alijitutumua kwa kujifanya kuuliza kama vile hakusikia alichoulizwa huku ni kweli alisikia sana!

    “Mimi siishi kwa undugu, naishi kwa ujirani mwema,” alianza kusema tena Hughes huku akirejea kutazama mbele bila kukitazama kioo, kwani alielewa Lana alianza kubabaika, “wajua kufahamiana ni habari yenye nafasi pana ambayo inaweza kuwa nzuri zaidi huku nikiwa sikatai inaweza kuwa uchungu wa shubiri.”

    Dereva aligeuka na kumtazama Lana, kisha aliachia kicheko kifupi, “dada si vibaya kumjibu mwenzako…nyote ni wateja zangu wazuri na ninashukuru mmekutana kwa staili hii, au ni vipi dadaa?”

    “Mimi si mkazi wa jiji hili, nahitaji kampani. Napenda kujuana na watu ili kupanua uhusiano nikiamini ni sehemu njema katika kukuza ujirani mwema.” Hughes aliendelea kusema, “Je, ni vibaya kufahamu waitwani? Ni vibaya kukufahamu dada yetu mrembo?”

    Huku akichekacheka, Lana alijibu, “Baba, maneno ni mengi…lakini sihitaji kukujua.”

    “Nisamehe dada, lakini sidhani ni vibaya watu kufahamiana…sisi si milima isikutane!” Hughes alijibu kinyonge huku bado akigoma kukubali kushindwa huku akijiambia alijidanganya kudhani tayari alilendemsha mtu.



    Hughes alizungumza maneno mengi hadi mwanamke alihisi kumuhurumia huku akijisemea moyoni, ‘si jina tu…ok, acha nimjulishe! Ila naogopa kusogezwa na huu uzuri wake! Hayo macho…mmh, naogopa miye!’

    Wakati huo walikuwa tayari wamefika nje ya nyumba ya Lana iliyopo mtaa wa Nera.

    “Dada, ninahisi nakuhitaji zaidi…lakini? Aah, sawa!” Hughes aliachia usemi wake wa mwisho huku tayari dereva akimuashiria kwa kumbonyeza pajani kwake, kwamba, asikate tamaa huku akimueleza kwa sauti ya chini sana, “kamua baba, usikate tamaa! Nitakutafunia baadaye!”

    Lana alitoa noti ya alfu tano na kumpatia dereva, na kabla ya kumuaga alimsisitiza ampitie usiku saa mbili; na ndipo alifungua mlango wa gari na kuanza kutoka taratibu huku Hughes akiendelea kumtazama na kuzidi kujionea uzuri mwingine huko katika makalio ambapo hakika ‘yalivimbiana’ vyema sana!

    Lana akiwa tayari nje, Hughes alisema tena, “dada hata hatuagani…yaani, kama vile tumekoseana mama?”

    “Hi! Baba wewe, kweli una maneno!” Lana alisema baada ya kugeuka mzimamzima kwa kujinyonganyonga.

    “Kama kufahamiana ni maneno, basi nisamehe dadaangu mrembo!” Bado Hughes alichomekea tena.

    Lana aligeuka tena mithili aliamua kumdharau Hughes; lakini alipopiga hatua mbili katika kuanza kuondoka, alisimama huku akikigeuza kichwa chake kiasi ili kumtazama dereva ambaye alikuwa akimzungumzisha Hughes. Alisema, “Kelvin, usisahau!”



    Lana Job alianza kuondoka akitembea kwa madaha huku macho ya Hughes yakimsindikiza kwa shauku huku moyoni akiamini bado nafasi ya kumnyakua ilikuwepo.

    Hughes alijisemea huku akivuta pumzi nzito, ‘if not somebody’s meal, I’ll die trying no matter what! (kama hana bwana, sitachoka kumsaka kwa hali zozote!)’



    “Huyo anaitwa Miss Lana.” Dereva alisema huku akipunguza mwendo katika kuuingia mtaa wa Selemani.

    “Miss!…ooh! Ok! Ok!” Hughes alijibu huku sauti fulani ikijipigapiga huko ndani ya mawazo yake katika kumjengea hoja asingelazwa makosani endapo angeendelea kumzozea Lana, ‘officially, she’s nobody’s meal!’

    “Kwasasa hana jamaa…tingisha!”

    “Yaap!”

    Hughes alifurahi sana!

    Akimuhisi vyema!

    Akimuhitaji vyema!

    Akikubali alisogea kumpenda pia!

    Kuanzia siku hiyo Hughes hakukubali kukoma, kwani kwa kumtumia Kelvin ndivyo alihakikisha alitengeneza mazingira ya kuwa karibu na dada huyo huku sasa akibadilisha aina za mawasiliano yake kwa kuamua kuwa mkimya huku akijua kuuweka mwili wake kuwa msemaji wa yote kupitia tazama zake hadi umaridadi wa uvaaji wake ili kuona ‘mlingoti wa mvuto wake’ aliusimamisha kwa tetemeshi zake; hivyo alifanya kwasababu alijua zilikuwepo njia mbalimbali za watu kuweza kuwasiliana huku akiipokea dhana kwamba njia kubwa zaidi za mawasiliano ni kwa njia za matendo na ishara za kimwili.

    Lakini si kwamba kwa muondoko huo, alipiga kisogo ‘kazi za kuchezea sauti’, la…hakusitisha; bali hivyo alipunguza ili kuzipatia nafasi pana zaidi vitendo na ishara mbalimbali zizalishwazo na mwili wake katika kuimarisha mvuto wake ili uweze kuwa mnenaji mwema asiyekuwa na makeke.

    Hivyo ndivyo alifanya!

    Hivyo ndivyo hata walijuana!

    Hivyo ndivyo hata walinasana huku bado kwanza akijua angekuja kumuacha baadaye kama ilivyo desturi yake katika kukamilisha ushindi wake!

    Ndio, waliweza kunasana kutokana na hulka zao kupatana. Kwani kule kutopendelea kwa Lana kueleza ni wapi angevutika zaidi katika kupatwa, huko kulikubaliana na hulka za Hughes kupendelea kuwa ‘msakakaji asiyeelekezwa’!

    Kwamba, Lana hakupenda kujulisha huku yeye pia akijua na kutambua wajibu wake wa kumsaka mwenzake!http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hivyo wote walisogezana kujifikisha kwasababu walijua ni jukumu la kila upande kufahamu mahitaji ya mwenzake kwa kuyatafuta kwa mwendo muafaka ndani ya raha zao katika kuzizidisha makali!

    Wote walijua wangetafuta wangeona kutokana na ishara za mawimbi ya uliaji, mawimbi ya upokeaji; kwamba, walijua ‘wangekunana’ huku kila mmoja akimsikiliza mwenzake ili kujisogeza hadi kun'gamuana hata kama si kwa kusafirishana katika ‘kufikishana’ ndani ya muda mmoja wakihema sawasawa!

    Ndivyo huko kulipeleka kunasana kwao hadi hatimaye kuwa ni wafikishanaji wazuri ndani ya muda mmoja huku wote wakimalizana wameridhishana bila minon’gono hasi!

    Hali hii na mengineyo ndio yalifanya Hughes ashindwe kujichomoa kama ilivyokuwa desturi yake; kwamba alishindwa kwasababu alibaini bado alimuhitaji Lana kwa dhati, na kadhalika alijongezwa kubaini kwa mara ya kwanza alimpenda mwanamke si kwasababu za tamaa za kingono tu!

    Na ndivyo hakukuwa tofauti kwa upande wa Lana ambaye hapo kabla alikosana na mpenzi wake kwa kule kutambua alikuwa na wake watatu na yeye akitakiwa kufanywa mke wa nne. Ndio, hakukuwa tofauti kwake, kwani alianza kujiondoa katika kumpenda Hughes kwa maana za kuburudishana kwa raha za muda ili kuingia katika kumpenda kwa dhati kadri ‘mahitaji yake’ alivyoona yakitimizwa; ndivyo pamoja na kujithamini, alizidisha kumpenda kutokana na hisia na kumuona Hughes akidhihirisha kumpenda huku wakati mwingi akimtamkia kwa mdomo kwa lafudhi za kimahaba.

    Kwamba alizidi kumpenda kila alipozidi kuhisi na kuona akithaminiwa, aheshimiwa huku akihisi dhihirisho zake mbele za kadamnasi, na akiona akihitajiwa na kutamaniwa sana kiasi akiuona uwepo wa mazingira kwamba alikuwa ni milki yake kutokana na kujikubali kwao katika kuelekea kuingizana huko ambako wasingeachana.

    Kwamba alizidi kumpenda alipozidi kuhisi na kuona Hughes alikuwa akiona fahari kumuita na kuwa naye karibu huku akihisi pia kama angehitajika kuchagua tena mpenzi, basi bado angechaguliwa yeye kwakuwa alionwa ni jambo la muhimu sana mbele za muhimu zake; na vyote hivyo ni kwakuwa aliona alichukuliwa kama rafiki wa karibu sana waliyeaminiana kwa dhati kiasi wangeweza kusameheana kama wangekosena kutokana na wote kujijali kama habari moja.

    Kwamba alizidi kumpenda Hughes kadri alivyomtia moyo, akimuunga mkono kihisia na kwa dhahiri hata mbele za watu kuhusiana na mtafaruku wake na mpenzi wake aliyepita ambaye Hughes alizoea kumuita ‘mzamani anayefurahi kuishi kizamani’; na ndivyo alifanywa kujiona mtu muhimu kuliko wote ndani ya maisha ya Hughes. Ni kwamba, kwa kuona na kujua huko alifurahi kukubali kwamba Hughes angesimama kidete kwa ajili yake wakati wa maumivu au matatizo kama ambavyo yeye pia alijichukua angekuwa mstari huohuo.



    Na si hivyo tu, kwani Lana alizidi kumpenda Hughes vile alivyompokea na kumkubali jinsi alivyo, na alifurahia zaidi kule kujiona akiwa ndani ya mipango ya maisha yake na utendaji wake; na pia alifurahishwa sana kwa kujua Hughes alikuwa ‘msasa’ usiyevurugwa na nguvu za mfumo-dume ambao alizoea kuuita, ‘primitive life style’.



    Hisia na mitazamo hiyo ya Lana ilijikuta ikiwa kiungo mzuri katika kuboresha uhusiano wao wa kimapenzi kiasi ndivyo Hughes alishindwa kujinasua kwasababu naye alikubali mahitaji yake yalitimizwa vyema kwa kudhihirika, kwani katika kushirikiana huko, ndivyo wote waligusana kwa mahaba na kubembelezana.

    Kwamba wote walipokeleana kwa shangwe hata ndani ya nafsi zao huku wakijiona wakiwa pamoja wakizidi kupendana hata mbele za walimwengu; na huku wakitiana moyo kwa kila jambo na kukukaribishana vyema kwa mawasiliano yote ya mdomo na namna zingine. Na zaidi walikubali walijua kutoshelezana na kuzawadiana vyema katika ‘kashkash za mapenzi’.

    Zaidi wote walijikubali walikuwa ni kimbilio jemana thabiti kwa kila mmoja wao, kwani kila mmoja alimuona mwenzake ni msaada mwema kwake kuanzia katika kuungwa mkono kwakuwa wote walijiona walikuwa ni wema na makini mbele za majukumu yao kuhusu uhusiano wao.

    Halikadhalika, walijipokea walikubali wasingeweza kuhatarisha uhusiano wao hata pale walipohitilafiana au kutokubaliana; na yote hayo ni kwa vile wote walijipokea walikuwa imara kwa ajili ya kuboresha uhusiano wao huku pia kila mmoja akimkubali mwenzake ni sehemu tulivu na laini ya kuangukia kwakuwa ni mahala pazuri penye kuvutia, ni mahala ambapo kila mmoja alikuwa hapendi kukosa kuwepo kwakuwa palikuwa ni mahala pa kujidai.



    Ndivyo hatimaye, Hughes alijikuta akishindwa kumuacha, kwani hata walifikishana hadi huko walioana; na kwa mwendo huo ilibidi Lana Job ahamishiwe kikazi jijini dar ili kumfuata mumewe!



    KATI YA MASURIA walioacha kazi kwasababu mbalimbali, ni Shabana ndiye alifanya Mrs Hughes kuwasiliana na mama yake mzazi aliyekuwa akiishi Singida kwa kaka yake ili kumtafutia mfanyakazi mwingine na kuja naye Dar-es-salaam.

    Shabana alikuwa ni miongoni mwa ‘housegirl’ ambao hawakuweza kukwepa ‘kichapo’ cha Hughes; lakini msichana huyu hakuwa ‘asusa kwa sana!’ kutokana na kutokuwa na vigezo vinono alivyohitaji mwanamke kuvimiliki. Hapo, Hughes alitulizwa kwa kupenda matiti yake madogo yaliyokuwa yamesimama wima huku akichukia kumuona akikosa ‘mbinuko’! Na ndivyo, alipenda kuishia kuzichezea titi zake na hivyo kujikuta akimtesa kiasi cha kumgeuza kuwa muendaji mzuri sana kwa mchumba wake ili kutulizwa ule ‘uchokozi’ ambao mara nyingi Hughes alikuwa haumalizi kila alipochokoza!



    Kama kawaida ‘uroho’ ulimchota Hughes siku alipomuona msichana huyo mpya wa kazi aliyekuja na mkwewe; ndio, alifurahi kwasababu alihisi alikuwa ni ‘mali’ isiyojua kuchezewa!

    Ni kweli hakukosea; huyo hakujua!

    Kwamba, huyo alikuwa hata hajui mfundishaji ujaje kwa hila zake ili hatimaye kutumbukizwa katika kumfanya kujikuta akiruhusu kufundishwa kucheza!

    Hatahivyo, Hughes hakupendezwa na ujio wa mkwewe. Lakini, si kwamba hakupendezwa kwa sababu za uchoyo; bali hakupendezwa kwa vile alijua ingekuwa kazi ngumu sana kuanzisha ‘vurugu’ kwa binti huyo aliyekuwa akiitwa Jacline. Hatahivyo, hakukata tamaa kwani alijua umakini wa hali ya juu ulitakiwa kuongoza mpambano bila kujenga ishara mbaya kwa mkwewe ambaye pia alikubali alikuwa bado ni ‘mali murua kuikandamiza’ kama angeona ilistahili kufukuziwa!

    Ndivyo, kwanza alizitafuta sababishi za kuwa karibu zaidi na binti kwa kujifunika ‘ushemeji mwema’; lakini, kadri alivyomsogelea ndivyo Jackline alizidisha kumuheshimu na hivyo kufanya ‘kazi’ kuwa ngumu zaidi! Halafu, zaidi hakujua kumbe upande mwingine ulikuwa pia ukinyemelea katika kufukuzia!





    Ndio, hakujua mama mkwe naye alianzisha tabia fulani zilizoashiria alikuwa mawindoni akiwinda kama ambavyo Hughes alivyokuwa akiwinda!

    Ndio, wakati wawili waliwinda!

    Ndivyo ilifanya wawili waliwindwa!

    Lakini bado ni mmoja tu hakuwinda!

    Lakini muwindaji aliwindwa pia!

    Yaani, kama Hughes alivyokuwa akimfukuzia Jackline, ndivyo yeye alifukuziwa na mkwewe!

    Ndio, mara nyingi mama mkwe alijipitisha mbele za Hughes huku mara kadhaa akiachia wazi baadhi ya sehemu zake za karibu na maeneo nyeti ili mradi tu macho ya mkwewe yashuhudie! Kwa mfano, wakati mwingine alijipitisha mbele zake, ama wakati akitokea bafuni huku khanga yake ikiwa imeloa maji na hivyo kushikana na mwili wake hasa katika zile sehemu za nyuma ambazo kusema kweli zilikuwa zikitikisika barabara kwani zilijaa vilivyo!

    Mwanzoni, Hughes alifikiri hayo yalifanyika kwa bahati mbaya, kwamba, hayo hayakukusudiwa; yaani, alifikiri pengine mama wa watu aliona yote ni kawaida tu isiyovunja sheria!

    Kumbe…kudadeki!



    ‘Mama anamchezea mamba? Mama niogope! Mama, shauri lako nikishindwa kudhibiti hali!’ Hughes alipata kuwaza siku moja mara baada ya mkwewe kumkalia katika kochi la mbele yake huku akitanua miguu kiasi cha aone huko ambako wala hakukuvishwa!

    ‘Mama nahitaji hiyo dogodogo! Huyo nikifika, naamini nimevumbua!…sio wewe mkomavu!’ Alijisemea zaidi huku akiinuka na kwenda zake chumbani, kwani hapo alikuwa ameketi katika mkao wa kuendeleza kujenga mazingira ya kutupa tazama zake kwa Jackline aliyemtuma amletee supu ya nyama.

    Naam, hakuona vyema tena kuendelea kuvuna ukodozi wake huo huku akijua pia Jackline angemfuata hukohuko chumbani kumletea supu yake, kwani siku hiyo mkewe hakuwepo.

    Hatahivyo, bado upande mkubwa wa mawazo ulin’gan’gania mkwewe asingekuwa na mipango ya kumpigania.



    ***

    Lakini vituko vya mama mkwe vilipozidi sana, Hughes alijikuta akigoma kufikiri pengine mtazamo wake ulidanganya; na ndivyo hata alianza kusogea zaidi katika kuamini ni hakika mkwewe alikuwa na agenda fulani aliyoificha ndani ya mawazo yake ambayo sasa ndivyo ilikuwa ikiachiwa ili kuhakikisha hatimaye kilichotakiwa kunaswa kishikwe.

    Yaani, mama huyu alimtamani…khah?

    Ni kuanzia hapo ndipo alianza kuona mkwewe alikuwa ni mshongo fulani aliyetamani kuzalisha ‘habari za mtu kumegewa kiwiziwizi’!

    ‘Kweli, mimi mlafi…but, she’s too much a munch!’ Mawazo yalimsafirisha huko wakati fulani alipokuwa amelala kitandani peke yake baada ya kupata chakula cha usiku; yaani, mawazo hayo yalimjia akimsubiri mkewe ili ‘wateremkiane kwa haki’.

    Na ndivyo kwa kuzielewa vyema hila za mkwewe, alijitahidi kuzipuuzia ikiwa ni pamoja na kutumia mbinu za kujaribu kujidanganya eti mkwewe asingeweza kuwa na dhamira hizo.



    Hughes alionyesha kumudu kukabiliana na hatua za mwanzoni za hila zake, lakini kitambo baadaye alijikuta akipunguza spidi ya kujidhibiti kutokana na kuzidi kuvutwa na matokeo ya kutazama umbo la mkwewe pale lilipowekwa ‘kihasarahasara’; ndio, alijikuta akianza kupenda kukodolea, kwani hakika mama mkwe alionyesha kutokata tamaa!



    Jinsi alivyozidi kushuhudia ugumu wa kumnasa Jackline, ndivyo mawazo yake yalianza kuvutwa na hisia za kuanza kumtamani mkwewe kiasi wawili hao kuanza kukaribiana ndani ya mawazo yao kwa kila mmoja kumuwaza mwenzake kinamna!

    Hatahivyo, Hughes hakuamua kuanzisha mpambano; bali alitulia akitazama kwa makini jinsi mwendo wa mkwewe ulivyokuwa ukimvumia huku akikaza dhibiti zake ingawaje hakutaka kuzikaza sana, kwani upande mwingine moyo wake ulikubali alikuwa ‘jimama’ ambalo bado hata katika umri huo lilikuwa na uwezo wa kumpeleka ‘puta’ mwanaume yeyote na ulijali wake!

    ‘Asingekuwa mkwe, ningemdunda!’ Hughes alijisemea hivyo mara kadhaa huku udenda ukitaka kumdondoka mithili ya mbwa mwenye haja.

    Hughes alimalizia kwa kujiuliza nini maana ya mapenzi, kwani bado ilimshangaza kuona mkwewe kuonekana kupanga mikakati ya kumsaliti mwanawe wa pekee katika kumpora mumewe!

    Alijiuliza kama mama alimtaka kwa mapenzi, au kama alimtaka kwasababu yeye pia ni mwanamke muhitaji kutibiwa na mwanaume!

    Hatahivyo, alikataa kutumbukizwa ndani ya kundi la watu wachache sana ambao wangeweza kusema hawajui maana ya mapenzi lakini huku wakikiri kuvutwa na mapenzi hayo; kwani bado alijikubali alikuwa miongoni mwa watu wengi sana ambao hushindwa kuelezea nini maana ya mapenzi, lakini bado, hatahivyo, wangeweza kusema wanajua mapenzi ni nini!



    VISA VYA MKWEWE vilimkumbusha Hughes habari zake za nyuma za kifuska katika ujana wake.

    Ndio, alitembea na binti kadhaa!

    Ndio, alitembea hata na dada zake!

    Ndio, alitembea na mijimama!

    Ndio, wakubwa kwa wadogo alibeba!

    Na bado, hata sasa ni hivyohivyo!

    Ndivyo John Hughes alipata wakati mgumu sana kuweza kujizuia hasiruhusu mkwewe kufanikisha hazma zake. Jitihada zake katika kujizuia huko zilikuwa si kwa sababu nyingine zaidi ya kuwa hakupenda kuruhusu kutokea jambo ambalo lingeweza kumuharibia maisha yake matamu aliyokuwa akiishi na mkewe, kwani uelewa wake ulimjulisha kumchezea mkwewe ilikuwa ni kuichezea shilingi katika tundu la choo; lakini bado aliona eti kuchezea ‘wengine’ haikuwa mbaya sana, kwani ilikuwa ni vyepesi kutubu kama mambo yangeharibika bila kubomoa ndoa yake!



    Hatahivyo, ni kweli hadi wakati huo tamaa zake zilianza kuhitaji kupewa nafasi ya kusaili mwili wa mkwewe; na ndio maana kuanzia wakati huo kila alipopewa nafasi ya kukodoa, ni hakika alifanya hasa!

    Huyo alikodoa hasa hata kama alifanya kwa mwendo mithili alitazama vya kawaida!



    ***

    Siku hiyo ya tarehe 21 ambayo iliangukia jumatatu, kituo cha polisi kanda ya kusini tabata kilipokea taarifa za mauaji yaliyoripotiwa majira ya saa tatu asubuhi kutokea kituo cha Usalama-Barabarani ambao walikuwa tabata baada ya kujulishwa habari ya ajali iliyotokea katika barabara ya mawenzi, huko tabata. Kwamba, gari dogo aina ya ‘toyota-limited’ iliyokuwa teksi-bubu ilikutwa imetumbukia daraja la kimanga; na ilikuja julikana kuwa taxi hiyo ilitokea mtaa wa damascus ambako pia ilisababisha ajali tatu! Kwanza, kwa kumgonga mtoto mmoja aliyekuwa akiuza vitafunwa mbalimbali pembezoni mwa mtaa huo katika makutano na barabara ya mawenzi; pia, hilo gari liliigonga gari nyingine ambayo nayo ilijikuta ikiuvaa ukuta wa nyumba moja kiasi wote katika gari ile ambao walikuwa ni familia moja walifariki papohapo!

    Ilisemekana dereva wa teksi hiyo alishindwa kumudu mwendo-kasi wa gari ambayo kabla ya kutumbukia daraja la kimanga iligonga na kuvunja ukuta wa nyumba moja!

    Askari wa usalama barabarani walifika eneo zote husika na ndipo hisia na tetesi mbalimbali zilianza kububujika kwamba dereva wa gari lile alikuwa pengine akikimbia jambo fulani ambalo walihisi lilitendeka ndani ya nyumba moja aliyokuwa akiishi Brigitte Mingly.

    Ni kwa mwendo huo ndipo ofisi ya upelelezi iliweza kufikishiwa habari hizo.



    ***

    Wakati huo taarifa hizo zikiletwa ofisi za polisi katika kanda ya Tabata mashariki, tayari Inspekta Hughes alikuwa ametulia ofisini kwake huku miguu yake kaitupa juu ya meza na yeye mwenyewe akijilaza kwa kukinyanyua kiti chake kidogo kiasi kiliegamia ukutani. Miwani myeusi aliyovaa ilificha ujulisho macho yake yalifumba; hatahivyo, hakulala.

    Mara simu ya mezani iliita!

    Aliisikia, lakini hakuichukua; aliiondoa miguu yake na kuituliza chini huku bado kaegamia kiti chake.

    “I’m tired, need some rest.” Alisema huku akikunja uso wake baada ya kuona simu ikiendelea kuita.

    Alikiweka kiti chake vizuri na kuketi vyema. Kisha aliondoa miwani yake na kuiweka mezani kabla ya kuuchukua mkono wa simu.



    Ni kwamba, mkuu wa kituo alimtaka John Hughes kwenda mtaa wa Damascus kufuatilia habari hiyo.

    Ndivyo Hughes na vijana wake waliwasili mtaa wa Damascus katika nyumba aliyokuwa akiishi Brigitte ambapo gari iliyosababisha ajali zote hizo ilisemekana ndipo ilitokea kwani kuna watu waliishuhudia ikiwa imesimama tangu mapema alfajiri; na zaidi, habari zilidai gari hiyo imekuwa ikionekana kuja hapo kwa marehemu mara kadhaa aidha ikimleta marehemu au ikija kumchukua hasa nyakati za asubuhi kwa ajili ya kumpeleka kazini.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hakukuwa na majengo mengi katika mtaa huo, na hiyo ilitokana na uwepo wa uwanja mkubwa wa kuchezea mpira ambao ulifuatia baada ya nyumba aliyoishi Brigitte ya ghorofa moja.



    Ndani ya sebule ya nyumba hiyo (marehemu aliishi ghorofani), alikutwa mtu mmoja akiwa kapigwa risasi tatu; yaani, risasi mmoja ilionekana ndio iliomtoboa vibaya mdomoni kwa kupitiliza katika mashavu yake mawili, na nyingine ilionekana kumpiga eneo la karibu sana na moyo wake huku ya mwisho ikiashiria kumvunja mbavu!

    Hatahivyo, mtu huyo hakufa!

    Alikutwa kazirahi!



    “Unamtambua?” Hughes aliuliza wakati wakiendelea kumuangalia mtu huyo.

    “Ndio afande. Huyu anaishi na Brigitte hadi sasa ingawaje siwezi kuthibitisha zaidi kwani huyu dada wakati mwingine simuelewi elewi!”

    “Afande!” Mtu mmoja alisema ghafla huku akitazama kwa makini sana michuruzi fulani ya damu ambayo ilielekea kujia mlangoni ingawaje haikuonekana kufika huko. Mtu huyo alikuwa miongoni mwa askari aliokuja nao Hughes ambao hawakuwa na mavazi ya kiaskari. Alisema zaidi mtu huyo baada ya kumpiga Hughes katika bega lake la kulia huku sasa akinyoosha kidole chake pale michirizi ilipoashiria kuanzia, “You see! Kama vile kitu fulani kilikuwa kikivutwa kama sio kilikuwa kikijivuta chenyewe! But…mmh, hapa ndio ukomo wake nadhani!”

    “I see.” Hughes alijibu taratibu huku akirudi nyuma karibu na mlango, “could be the run of driver! (inawezekana ni dereva alipokuwa akikimbia!)”

    Yule mtu alitoka nje ya nyumba na kutazama tazama sakafuni, na baadaye kidogo alirudi huku akivuta juu mabega yake kabla ya kuchezea sharubu zake.

    “Afande sidhani kama utakuwa ni mburuzo wa mtu kujivuta…aah, tuwaachie wapima alama kwanza. Hii michirizi…mmh, si ya huyu mtu…someone else!”



    Katika chumba kimojawapo kilichokuwa jirani na sebule, huko ulikutwa mwili mmoja ukiwa bila kichwa!

    “Aay? Afande, huyu ndiye Brigitte! Maskini, unyama gani huu ametendewa! Wallahi…aah!” Mjumbe wa mtaa aliyekuwa akiitwa Mashaka alisema kwa masikitiko baada ya kukiona kichwa cha mtu kikiwa umbali kidogo na ule mwili waliouona wakati wakiingia chumbani.

    Inspekta alitingisha kichwa.



    Waliingia chumba ambacho kwa jinsi kilivyokuwa waliweza kubaini ndicho kilikuwa chumba cha kulalia cha marehemu Brigitte, na kisha walielekea kule yalipokuwa makabati mawili ya nguo huku mazungumzo ya hapa na pale yakiendelea hadi pale wapojikuta wote wakikatishwa na mshtuko mdogo aliouonyesha Inspekta Hughes mara walipofikia makabati yale!

    “Look! Hili limevunjwa!” Inspekta alisema huku akigeuza kichwa chake kumtazama askari aliyekuwa karibu yake. Huyu alivaa kiaskari.

    “Ni kweli afande!” Askari yule alijibu bila kumtazama Inspekta; na tayari alianza kukagua milango ya kabati hilo, kwani mikononi alivalia glovu.

    Mlango wa kabati hilo ulipoguswa tu, ukafunguka kirahisi na kuonyesha ni kweli haukufungwa!

    “Ulitegeshwa!” Askari yule alisema huku akitazama chini alipoona kipande kidogo cha karatasi kilichoanguka mara baada ya mlango kufunguka.

    “Ni kawaida hii?” Hughes aliuliza huku akisogea zaidi.

    “Huenda, lakini sidhani. Inawezekana upo uhusiano na hili tukio…ni wizi? Hapana, hili hatuwezi kusema sasa.” Yule askari alishauri huku akikiokota kipande kile na kukitumbukiza ndani ya mfuko aliokuwa nao mara baada ya kukigandisha na karatasi yenye gundi aliyoiandika juu yake alama maneno fulani ya utambulisho.

    Upekuzi uliendelea…



    Hughes alichukua nyaraka kadhaa ikiwa ni pamoja na faili moja lililohifadhi picha; lakini tena alijikuta akishtuka baada ya kuuona mfuko fulani uliotuna!

    Huo hata ulianguka chini!

    Wengine nao wakashangaa, kwani vilivyodondoka vilionekana! Zilikuwa ni idadi kadhaa za hirizi zenye ukubwa tofauti tofauti, zote zikiwa zimefungwa kwa kitambaa cheusi…mmh?



    “Mzee, ulisema marehemu Brigitte aliwahi kuishi hapahapa na mwanaume mwingine…je, unazo habari zozote kuhusu mtu huyo?” Hughes alimuuliza Balozi; na hapo walikuwa wakielekea katika kabati jingine…

    “Habari? Zipi hizo unauliza Afande?”

    “Habari kama…mfano wajua nini kilitenganisha?”

    “Unajua afande, yule jamaa ni mtu wa ajabu sana.” Alianza kujibu Mzee Mashaka, “karibu watu wote humshangaa sana…eeh, kwanza ningekufahamisha hili. Inasemekana jamaa ndilo mume halali wa marehemu.”

    “Hold on! Hold on a bit!” Inspekta aliwahi kabla mzee Mashaka hajaanza kuendelea tena.

    Mzee alimtazama Hughes kwa macho ya usikivu.

    “Unasema inasemekana au ilisemekana?”

    Mzee Mashaka alitazama pembeni, akasogea mbele hatua mbili tatu hivi. Kisha aligeuka tena na kumfuata Inspekta huku akitabasamu.

    “Labda niseme hivi.” Alianza kusema tena mzee huyo, “watu wengi wanadai kumsikia Brigitte…ooh, Mungu nisamehe, kwani sipendi kuongelea mabaya ya marehemu!”

    “Wala humsemi marehemu vibaya, bali watumia wajibu na haki yako kuisaidia polisi katika kutekeleza majukumu yake…you’re duty bound publicly!”

    “Thanks. Unajua afande…ooh, eti uliniuliza nini?”

    “Umesema huyo mtu ndiye mume halali wa marehemu kwa habari za kusemekana. Au sivyo?”

    “Afande watu wengi wamewahi kumsikia marehemu mwenyewe akitamka kuwa huyo ndiye alikuwa mumewe halali. Hao wengine kama huyo marehemu tuliyemkuta barazani walikuwa ni wezi.”

    “Huyo mwanaume bado hatujajua kama tayari ni marehemu, kwani zipo ishara anaweza kuwa bado anapumua.” Hughes alisawazisha kidogo na kuachia tabasamu jepesi.







    “Nyie wataalamu, sisi hatuwezi kujua hayo…lakini, kupona huyu sidhani! Kajeruhiwa vibaya sana!”

    “Ok. Hayo tuwaachie madaktari,” Hughes alinyamaza kidogo na kisha tena aliendelea, “unajua sijakuelewa unaposema huyo mtu alikuwa ni miongoni mwa wezi. Kivipi? Kwa wizi upi? Hao wengine unazo habari zao?”

    Inspekta Hughes aliuliza swali hilo katika kutaka kuhakikisha vile alivyoelewa kama ndivyo mwendo ulikuwa katika kuanza kuichambua tabia ya marehemu.

    Balozi Mashaka alijibu kwamba Marlon hakuwa mume halali wa marehemu.

    “Ndio maana mzee nahitaji kufahamu habari zaidi za huyu unayesema ndiye mumewe…kwanza anaitwa nani na unaweza kujua wapi anaishi kwa sasa?”

    “Ni Henry. Anaishi Bunju.”

    “Unaweza kunieleza kwa ukamilifu?”

    “Ukamilifu upi afande?”

    “Full particulars of his whereabouts.”

    “Specifically, I don’t know. Ila baba mwenye nyumba anaweza kupafahamu vizuri…nitakuelekeza nyumbani anapoishi. Not far from here.”

    “Ok. Hivi…unaelewa lolote kuwa waliachana…ooh, yaani, hao walitengana kwa sababu gani?” Hughes aliuliza tena huku akiandika katika kidaftari kidogo alichokitoa katika mfuko wa shati lake pamoja na kalamu.

    “Unajua jamaa ni mvumilivu sana kama sio sahihi nikimsema ni bwege wa karne hii!”

    Inspekta aliendelea kusikiliza.

    “Hivi uliona wapi mke wa mtu kurejeshwa nyumbani na wanaume usiku wa manane, halafu mume huyohuyo ndiye amfungulie mlango bila kufanya purukushani?”



    ***

    INSPEKTA HUGHES aliendelea kumsikiliza balozi.

    “Hivi uliona wapi mke wa mtu kurejeshwa nyumbani na wanaume usiku wa manane, halafu mume huyohuyo ndiye amfungulie mlango bila kufanya purukushani?” Mzee Mashaka alisema tena, na kisha aliendelea kwa kulijibu swali lake mwenyewe na hivyo kuashiria alitaka kulijibu mwenyewe, “basi hao ndivyo waliishi kabla ya kuja kuachana. Hili ni jambo kila mtu mtaani alijua wangefikishana kuachana.” Alinyamaza kwa muda, na kisha tena aliendelea, “kwanza, tulidhani alikuwa hajui…kumbe alikuwa akielewa kila kitu kulingana na maelezo yake mwenyewe mara tuliposhindwa kunyamaza kimya!”



    Mzee Mashaka aliendelea kumhadithia Hughes kwamba kilichofanya hadi kufikia kutengana kwao ni pale uchumi wa jamaa (Henry) ulipoporomoka.

    “Awali inadaiwa marehemu alikuwa hachelewi kurejea nyumbani, kwani kama alichelewa basi ni kwakuwa wote wawili walikuwa nje wakiwa pamoja.”

    Hughes alielezwa kuwa kadri Henry alivyokuwa akiporomoka kiuchumi, ndivyo marehemu alizidisha tabia za kurejea nyumbani usiku wa manane kama sio kurejea alfajiri au hata zaidi ya hata siku mbili!



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog