Search This Blog

Monday 24 October 2022

WIMBO WA GAIDI - 5

 









    Simulizi : Wimbo Wa Gaidi

    Sehemu Ya Tano (5)





    Ni pesa ambayo hakutaraji kuimiliki maishani mwake. Na sasa ilikuwa inamnyenyekea yeye. Aifanye atakavyo. Tabasamu zuri likajijenga usoni kwake. Akaichomoa ile kadi, akaiweka mfukoni kwake na kurudi pale hotelini.

    “Umeridhika sasa Brey Jabba?” Zidadu alimuuliza. Brey akatabasamu.

    “Kwa sasa nimeridhika…lakini najua bado kuna zaidi…” Alisema.

    “Ni kweli, lakini kama ulivyoelekezwa, utakuwa unaingiziwa hela zaidi kwa awamu kadhaa wa kadhaa…ili kuondoa mashaka…”

    “Okay. So nini kinafuata?”

    “Kifuatacho tunaondoka hapa hotelini. Tunaelekea kwenye makazi yako mapya Brey, na maisha yako mapya…kama mkuu wa usalama kwenye kile kiwanda, na utakuwa unakaa nyumbani kwangu kama mpwa wangu…” Zidadu alimwambia.

    “Dah, kwa hiyo huu ndio mwisho?”

    “Ndio mwisho huu…kazi yako imekamilika, na nashkurua kuwa umefika salama. Huko tuendako hakuna atakayekujua wala kukubughudhi.”

    “Oh yeah…sasa na hela kama hii naitumiaje huko maporini?” Brey alisema.

    “Ni juu yako…lakini usiwe na haraka…inabidi upotee hata kwa mwaka mzima kwanza…ingawa ingebidi usishie huko huko tuendako tu.”

    “Ah, tutaona juu ya hilo…”

    Kimya kilipita kidogo.

    “Kwa hiyo…wewe ni nani haswa, ukiachilia mbali kuwa jina lako ulilonitajia ni Zidadu?” Brey alisaili, udadisi ukimzidi. Na yule bwana akacheka kidogo.

    “Hunikumbuki kabisa?” Alimuuliza, na Brey akakunja uso.

    “Mi ndo kwanza nakuona leo…nikukumbuke from where?” Alimuuliza kwa makini, akimaanisha amkumbuke kutokea wapi?

    Zidadu alimung’unya midomo na kutikisa kichwa kwa namna ya kujiafikia jambo akilini mwake.

    “Ndio nini sasa hiyo…natakiwa niwe nakufahamu?” Alimuuliza.

    “Inabidi tuondoke hapa Brey…bado ni mjini hapa. Unavyokuwa nje ya miji mapema kadiri iwezekananavyo, ndivyo unavyokuwa salama kwa uhakika zaidi.” Jamaa alimjibu. Brey akakunja uso.

    “Mbona sikuelewi? Hujajibu swali langu…”

    “Hukutakiwa uwe unanifahamu tena sasa…”

    “What do you mean sikutakiwa niwe nalufahamu tena?”

    Mgina akaguna.

    “Ndio hivyo…hutakiwi uwe unanifahamu kutokea huko nyuma, lakini kiufupi Brey, mimi ni mmoja wa walioshiriki kukufanya hivi ulivyo…”

    “Whaat?” Brey alimaka.

    “Oh, yeah…na ninanjivunia sana kwa hilo.”

    Brey alimtazama, akikumbuka namna hayati Benson Kanga alivyoonesha kumakinika na hali ya kuwa hakuweza kumkumbuka ilhali sauti yake ikiwa si ngeni masikioni mwake.

    Kuna uhusiano gani hapa?

    “Unahitaji kufafanua zaidi hapo aisee...” Alimwambia.

    “Ni hadithi ndefu…lakini nadhani tungeanza kuondoka sasa hapa. Elewa kuwa niko upande wako.” Zidadu alizidi kumchanganya.

    “Nina muda mwingi tu wa kusikiliza aisee…niambie zaidi!”

    “Tutakuwa tunaishi nyumba moja Brey, haraka ya nini? Tutapata tu muda wa kuongea juu ya haya…rudisha chumba tuondoke aisee…” Zidadu alisisitiza.

    Lah!

    Dakika kumi na tano baadaye walikuwa kwenye gari aina ya Toyota Stout ya kizamani lakini yenye nguvu kama mpya, wakielelekea nje ya mji…



    ***





    Ulikuwa ni usiku mkubwa walipofika kule kijijini, na Zidadu akaenda naye moja kwa moja hadi nyumbani kwake, ambako kutokea pale nyumba ile ilipokuwa, aliweza kuliona eneo kubwa linalomilikiwa na kiwanda kile kutokea juu.

    “Nadhani leo upumzike…kesho utaripoti huko kazini kwako…na wale jamaa watakupatia nyumba mule mule ndani ya eneo la kiwanda, na humo tutakuwa tunaishi sote…” Zidadu alimwambia.

    “Na vipi kuhusu hii nyumba tuliyomo sasa?” Brey aliuliza.

    “Hii ni nyumba yangu binafsi…nayo tutakuwa huru kuitumia muda wowote. Utakaa kule ndani, kisha utanialika na mimi kama mjomba wako kuja kuishi mle…ni muhimu tuwe pamoja kwa muda mpaka angalau utakapozea mazingira, kisha mimi naweza kurudi hapa kwangu…” Zidadu alimwambia.

    “Kwa nini ni lazima tuwe sote kule?”

    “Ah, kwenye medani za kiusalama wa aina hii…kuna watu wanaoitwa “operatives” Brey, yaani watekelezaji wa operesheni maalum ya kiusalama…kwenye hili swala ulilotoka kulitimiza, huyu “operative” ni wewe. Na kila operative anatakiwa awe na “handler”, yaani mdhibiti wake, na kwenye hili swala huyo handler ni mimi. Sasa ni lazima handler na operative wawe pamoja kwa muda hususan baada ya kumalizika kwa operesheni kubwa na ya hatari kama hii uliyotoka kuitekeleza wewe…” Zidadu alifafanua.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Yaani unataka kuona iwapo ile kazi niliyopewa haijaniathiri kisaikolojia au vinginevyo…au haijanifanya niwe tishio kwa taifa na kwa wengine, sio?” Brey alimuuliza, na kabla Zidadu hajajibu, akaendelea, “…na kama ukiona kuwa naelekea kuwa tishio…unaniua.”

    Halikuwa swali.

    Zidadu akamkodolea macho, na kwenye macho yake Brey akauona ukweli.

    “Don’t worry mjomba…niliyajua yote haya wakati nakubali kuingia kwenye operesheni hii…sitakupa nafasi ya kufanya hivyo anko…”

    “Hizi kazi hazina muamana Brey, na siwezi kukubishia wala kukukatalia juu ya hilo…lakini elewa, wewe ni zao langu ninalojivunia sana…si lolote kama hilo linaweza kutokea kwako, kama nitaweza kuliepusha.”

    Brey alimtazama tu bila ya kutia neno zaidi. Ghafla alihisi uchovu mkubwa. Aliamua kuliacha hilo kwa muda ule. Alielekezwa kwenye chumba chake, naye akajifungia humo na kulala.



    _________________



    Asubuhi ya siku iliyofuata alikuwa tayari kwenda kuripoti kwenye kazi yake mpya.

    “Pale utakuta uongozi unakutarajia, hivyo wewe utaenda nao kwa kadiri ya hali utakayokutana nayo pale…hivyo vyeti na “CV” yako ndivyo ambavyo wao wanavyo kwenye mafaili yao pale.” Zidadu alimwambia.

    “Ina maana na wao wanajua ukweli kuhusu mimi?”

    “No way. Wao wanajua kuwa wewe ni afisa wa usalama mzoefu tu, si zaidi. Wale ni wawekezaji, na moja ya masharti waliyopewa na serikali ni kuajiri wazawa, na ndio maana wafanyakazi wengi wa kile kiwanda ni wazawa tena wa maeneo haya haya ya kijiji hiki na vile vya jirani…yaani kwa ufupi wengi ni washamba tu pale. Ni moja ya sababu kwa nini ilibidi uje kukaa huku...hakuna atakayekutambua wala kukufuatilia huku…”

    “Sasa ilikuwaje wakafikia uamuzi wa kunichagua mimi…?”

    Zidadu akacheka kidogo.

    “Yaani seriali iliwapa sharti kwamba nafasi ya mkuu wa usalama hapa lazima atoke serikalini na ni serikali ndiyo itakayomleta. Jamaa hawakuwa na jinsi. Walikufanyia usaili kwa simu tu, ambapo kuna mtu aliyekuwa akijibu maswali yao kwa hiyo simu, wao wakiamini kuwa ni wewe…serikali ikitaka lake haishindwi bwana.”

    Brey akapiga kimya.

    “Na vipi wakiamua kufuatilia habari zangu kwenye hizi kampuni nyingine duniani mlizozinadi kuwa niliwahi kufanya kazi za ukuu wa usalama huko? Watagundua nini?”

    Zidadu akacheka tena.

    “Yaani huu mtandao uko dunia nzima…ni ushirikiano wa serikali kadhaa…sasa wao wakipiga simu kwenye hayo makampuni, ile simu itaelekea sehemu tofauti ambapo atakayepokea atampa maelezo hayo hayo yaliyomo kwenye hiyo CV…lakini niamini mimi, hawatafuatilia hilo...wao wameishukuru tu serikali kwa kuwapatia mtu wa usalama kwenye eneo lao…”

    Brey akaguna.

    “Isitoshe…hakuna kazi yoyote iliyo muafaka kwako kwa sasa zaidi ya hiyo Brey…ni kazi pekee inayokuhalalishia kutembea na silaha wakati wote. Zaidi ya hapo, huwezi kukaa tu bila kazi ukijificha huku kijijini, na wakati huo huo uonekane unafanya matumizi kadhaa wa kadhaa ya hela…hata bwege atajiuliza unapata wapi hizo hela…lakini ukiwa unaonekana ni muajiriwa kwenye kiwanda kikubwa na kinachoheshimika sana eneo hili kama kile, hakuna atakayehoji…” Zidadu akafafanua zaidi.

    Brey akapiga kimya, akiyazamisha yote yake akilini mwake.

    “Okay, wacha niende…bado tuna mengi ya kuongea, mimi na wewe.” Alisema huku akiinuka kutoka mezani walipokuwa wanakunywa chai.

    “Najua…na muda tunao sana tu. Wacha nikupeleke…” Zidadu alisema, na dakika chache baadaye walikuwa garini, akipelekwa kwenye ajira yake mpya.

    __________________



    Anand Timber Mill kilikuwa ni kiwanda kikubwa kilichojichmbia pembezoni kabisa ya kijiji kidogo kilichopo wilaya ya Kilolo. Kulikuwa kuna shamba kubwa sana la miti, ambalo lilikuwa likimilikiwa na kiwanda kile, miti ambayo ilikuwa ikipandwa, ikihudumiwa na ikivunwa kwa ajili ya kutoa mbao madhubuti kabisa kwa ajili ya kusafirishwa sehemu mbali ndani na nje ya nchi. Kama alivyoeleza Zidadu, kile kiwanda pamoja na lile shamba lake kubwa kabisa kilikuwa kimeajiri wafanyakazi wasiopungua elfu moja, wengi wao wakiwa ni wazawa na wenyeji wa kile kijiji na vijiji vya jirani na hata wengine wakitokea sehemu nyingine za Iringa na mikoa ya jirani.

    Zidadu alimuacha getini kisha yeye akageuza, na Brey akajitambulisha pale getini akionesha barua yake ya ajira na kupelekwa moja kwa moja hadi kwa mkurugenzi mkuu wa kiwanda kile, jamaa mwenye asili ya kihindi. Ndani ya saa chache tayari alikuwa ameshaelekezwa mahala ofisi yake ilipokuwa, akakabidhiwa gari aina ya Suzuki Maruti ya muundo wa “kibandawazi”, lenye nembo ya kiwanda kile ubavuni, na kuambiwa kuwa lile ndilo lingekuwa gari lake la kazi. Akaoneshwa nyumba nzuri sana iliyojengwa kwa mbao tupu, iliyokuwa ndani ya eneo la shamba kubwa la kiwanda kile, akiambiwa kuwa pale ndipo atakuwa anaishi.

    “Mkeo anakuja lini, bwana Jabba…? Kuna maelekezo inabidi apewe kuhusiana na namna ya kufanya upishi humu ndani, si unajua hii ni nyumba ya mbao tupu?” Afisa tawala wa kiwanda alimuuliza wakati anamkabidhi ile nyumba.

    Brey akacheka.

    “Nielekezeni mimi tu…sina mke kwa sasa…ila mjomba wangu, anaweza kuja kuishi nami hapa…” Alimjibu.

    “Oh? Okay si tatizo…” Jamaa alimjibu na afisa mwingine akampa maelekezo ya namna ya kutumia majiko yaliyokuwa mle ndani.

    Kwisha kufanya mambo yote hayo akatambulishwa kwa wafanyakazi wote pale kwenye mkutano maalum uliohusisha wafanyakazi wote, na baada ya hapo meneja wa kiwanda akamzungusha eneo lote la kiwanda kwa gari, hadi kule kwenye lile shamba kubwa kabisa. Siku yake ya kwanza iliishia kwenye kulizungukia eneo lililokuwa chini ya himaya yake kiusalama, akiwa anawajibisha askari kadhaa wa ulinzi pale kiwandani na wasaidizi wa ofisini wawili.

    Ndani kabisa ya moyo wake, alijiweka tayari kuanza maisha mapya…akijiapiza kusahau yote aliyopitia huko nyuma ikiwemo yale aliyotoka kukabiliana nayo jijini Dar siku mbili tu nyuma.

    Kwa picha aliyoiona kwa siku ile ya kwanza tu kazini, alihisi kuwa hilo lingekuwa ni jambo jepesi sana, kwani mazingira yalikuwa muafaka sana kwake. Na kama alivyosema Zidadu, hakuona dalili ya mtu yoyte kuweza kumtambua akiwa pale kijijini.

    Ndivyo alivyoamini...



    _________________



    Na ndivyo ilivyokuwa mwezi mzima baadaye. Hakukutana na jambo lolote la kumrudisha kwenye maisha aliyokuwa akiyaishi kwa miaka kadhaa huko nyuma. Maisha ya kutembea akiwa roho mkononi, kila muda tayari kwa kukabiliana na mtu mwenye lengo la kuyadhuru maisha yake. Lakini hakupoteza umakini wake.

    Waliishi na mdhibiti wake Zidadu kwenye ile nyumba aliyopewa na kiwanda kile alichokuja kukubali kuwa kilikuwa kikiheshimika na kuthaminika sana pale kijijini na hata mkoani.

    Hakika alikuwa akielekea kuwa binadamu wa kawaida, jambo alilokuwa akilitamani kwa muda mrefu. Mashetani ya umwagaji damu ndani yake hatimaye yalikuwa yamelala.

    Alifanikiwa kumdodosa zaidi Zidadu kuhusu yeye na namna walivyokutana.

    “Brey, tosheka na ukweli kuwa nilikuwa mkufunzi wako kwenye hizi kazi…hili la kuwa kuna vitu huvikumbuki maishani mwako sio geni kututokea kwenye kazi hizi…ni namna ya akili yako kutaka kutokumbuka sehemu fulani ya maisha yako ambayo ni mbaya…sijui lakini…ila ndio maana mimi niko na wewe…”

    Brey alilitafakari hili jibu na akaona halimuingii akilini. Hakutaka kubisha zaidi, bali akaliwekea maamuzi ya kulipeleleza kwa kadiri atakavyoweza, akiwa na yule “mdhibiti” wake.

    Maisha yalikuwa mazuri tu pale kijijini. Ndani ya mwezi mmoja tangu afike pale kijijini, walishatembelea sehemu mbali mbali za kijiji kile, wakifurahia mandhari maridhawa ya kijijini pale, wakienda kwenye matukio mbali mbali ya harusi na misiba ya majirani au hata baadhi ya wafanyakazi wenzake pale kiwandani, na mara zote hizo hakukuwa na hata dalili ya kutambulika au kutokea mtu wa kumfuatilia.

    Mpaka jumapili moja walipoamua kwenda sokoni kufuata mahitaji yao ya pale nyumbani…





    _______________



    Walifika sokoni asubuhi ile na kufanya manunuzi yao mumimu, wakaweka garini vifaa vyao walivyonunua. Brey akagundua kuwa kulikuwa kuna watu wengi sana siku ile pale sokoni, kinyume na ilivyokuwa jumapili iliyopita, naye akamakinika na hali ile kikawaida tu.

    “Mnh, mbona leo watu wengi sana sokoni…ni kawaida kweli hii?” Brey aliuliza. Zidadu akacheka.

    “Leo ni zamu ya kijiji chetu kuendesha gulio…” Alimjibu.

    “Zamu ya kijiji chenu…?”

    “Yap! Ni kawaida kuwa kila mwezi, kwenye jumapili ya mwisho wa mwezi, huwa kuna gulio kubwa kwenye kijiji kimojawapo miongoni mwa vijiji vilivyo jirani na hiki chetu…yaani hili gulio huzunguka kutoka kijiji kimoja kwenda kingine kila baada ya mwezi mmoja…sasa naona leo ni zamu ya kijiji hiki.” Zidadu alifafanua. Brey akatikisa kichwa.

    “Yaani hadi leo bado kuna mambo haya? Ama kweli huku kijijini…” Alisema na Zidadu akacheka tena.

    “Ndio maisha ya kijijini haya tena…inabidi uyazoee na ujichanganye nayo sasa…”

    “No way! Sijizoeleshi mambo kama haya. Twen’zetu bwana!” Brey alimbishia huku akicheka.

    “No, sio mbaya tukazurura kidogo...uone mazingira haya…hakuna lolote la maana tutakalokuwa tunaliwahi huko nyumbani saa hizi…” Zidadu akamshawishi. Brey akasita kidogo, kisha akakubaliana naye. Wakaanza kuzurura miongoni mwa vibanda kadhaa vya bidhaa mbali mbali, wakiangalia hiki na kile, mara wakiuliza bei ya hiki na ya kile, alimuradi walikuwa ni miongoni mwa wananchi waliokuwa wakifurahia jumuiko lile litokealo mara moja baada ya miezi kadhaa pale kijijini.

    “Unaonaje tukapata na mlo wa mchana huku huku…hii kujipikia kila siku nayo inachosha, bwana…au vipi?” Zidadu alimuuliza huku wakiendelea kurandaranda gulioni, wakijipenyeza miongoni mwa watu waliokuwa wakipita huku na huko.

    “Kama kutakuwa kuna wali wa maharage basi umenipata! Yaani katika mlo usioniisha hamu ni huo kaka!” Brey alisema na Zidadu akamcheka zaidi.

    “Na hasa ukizingatia kuwa hukuwa umeupata kwa muda mrefu…”

    “Basi ndio kabisaaa!” Brey aliunga mkono, wakacheka. Maisha ya kawaida yalikuwa yanaelekea kuwa murua sana kwake.

    Walikuwa wakipita kwenye msongamano wa watu huku wakisuguana mabega na wale waliokuwa wakipishana nao, kelele zikiwa zinavuma kutokea kila kona. Wao hawakujali, walizama kwenye mazungumzo yao.

    “Okay, basi hilo limepita maana hapa kuna mama ntilie wa kila mlo, lakini maharage ni garant…” Zidadu alikuwa anamwambia, lakini hakuwahi kumaliza kauli yake.

    “Bichei!” Sauti kali ya kike iliita karibu sana na wao, na sanjari na muito ule Brey aliona kwa pembe ya jicho lake kitu kikimuelekea pale alipokuwa, hakujua mara moja kama kile kitu kilikuwa ni mkono au rungu au fimbo.

    “HEY!” Alimaka kwa mshituko huku akijizungusha kukikwepa kile kitu, na hapo akakoswakoswa na kiganja cha mkono wa binadamu kilichokuwa kikimuelekea aidha begani au shingoni au mgongoni.

    “Heeh, hebu tulia! Mkamateee!” Sauti nyingine ya kike ikarindima muda ule ule, sanjari na sauti ya Zidadu iliyokisikia ikisaili kulikoni.

    “Nini pale tena?”

    “No! BICHEI! BICH…BICHEI WANGUUU….!” Ile sauti ya kwanza ikapaazwa tena. Brey akageuka kwa wahka kule ilipotokea ile sauti, na akajikuta uso kwa uso na mwanadada wa makamu, akiwa ametumbua macho hali povu likimtoka kinywani, akimtazama moja kwa moja usoni huku akimuoneshea kidole.

    “Bicheiii! Bicheiii…!”

    Hata pale alipokuwa akimshangaa yule mwanadada aliyekuwa akimpigia kelele huku akilitamka lile neno lisiloeleweka na akimnyooshea kidole, aliona mwanamke mwingine mtu mzima zaidi akiwa amemshika kiuno kutokea nyuma yule mwanadada, uso akiwa umemhamanika vibaya sana.

    “Nisaidieni jamani…mgonjwa huyu! Mkamateni!” Yule mama alikuwa akisema kwa taabu huku akibishana na yule mwanadada aliyekuwa akijikukurusha kutoka kwenye himaya ya yule mama, akiwa anataka kumfuata Brey pale alipokuwa.

    Aka!http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Zidadu aliruka mbele haraka na kumkinga Brey.

    “Nini hii? KWA NINI ANAFANYA HIVI?” Brey alimaka.

    “Densa kichaaa kalipuka!” Mtu mmoja alipayuka kutoka miongoni mwa wanakijiji waliojaa pale kushuhudia kile kilichokuwa kinatokea, na Brey akamuwahi na kumkamata mkono yule aliyesema maneno yale.

    “Kichaa?” Brey alimhoji, na kabla yule jamaa hajajibu, Zidadu akamshika na kumvutia pembeni, kumuweka mbali na kile kilichokuwa kinatokea.

    “Inaonekana hivyo aisee…tuondoke!” Alisema, na Breya akahisi mlipuko kichwani mwake, kiza kikamtanda akilini kwa muda, kisha kila kitu kikarudi kama kawaida.

    Alihamanika kweli kweli.

    Aligeuka kule nyuma huku akimfuata Zidadu kule alipokuwa akimuongoza. Watu walikuw wamemzonga yule mama na yule dada aliyekuwa naye, na sasa alisikia makelele makubwa zaidi kutoka kwa yule dada aliyesemwa kuwa ni kichaa.

    Alimkamata dada mmoja aliyekuwa akikimbilia kule kwenye lile kundi la wanakijiji lililomzonga yule mama na yule dada.

    “Ni nini pale? Yule dada…unamjua?” Alimuuliza kwa wahka. Dadaa akacheka.

    “Dada chizi yule…!” Binti alimjibu, akaendelea, “…anatokea kijiji cha jirani hapo….huwa tunamwita densa kichaa…kwa mauno huyo! Heeeeee-heh!” Binti alimjibu kisha akakimbia huku akicheka.

    Ebbo!

    Brey akamgeukia Zidadu.

    “Yule kichaa…kanitamb…?” Hakumaliza, kwani muda huo mayowe yakazidi, na hata pale wote wawili walipokuwa wanageukia kule zile kelele zilipokuwa zinatokea, walimuona yule dada kichaa akiwa anawakimbilia pale walipokuwa hali raia wengine wakimkimbiza.

    “Hey! Nini kinaend…” Brey alimaka, lakini Zidadu akawahi kuruka mbele kwa wepesi wa ajabu na kumkabili yule dada, lakini kwa mshangao wa wote pale, dada alijirusha mbele na kuserereka mavumbini, akajibinua kwa namna iliyomfanya Zidadu aruke pembeni kumkwepa, na alipogeuka yule binti alikuwa ameshamfikia Brey. Brey aliruka pembeni tayari kumtupa hewani kwa judo kali yule dada, lakini binti alisimama ghafla mbele yake, akamtazama moja kwa moja machoni, kisha akamnyooshea mkono kama vile askari wa usalama barabarani afanyavyo anapotaka kusimamisha gari.

    Brey akasita.

    Hapo hapo yule dada akaanza kucheza dansi kwa namna ya ajabu kabisa, mkono mmoja akiwa ameunyoosha mbele kama aliyeegemea kitu ilhali hakuwa ameegemea chochote, akaanzaa kukata kiuno kwa mtindo wa kuvutia sana huku kwa wakati huo huo akiidonoa-donoa ardhi kwa ncha za vidole vyake kwa namba ya kuvutia kabisa.

    “WEWEEEEEE!”

    “OYA OYAAAA”

    “WERA WERAAAAA!”

    Raia walishangilia kwa fujo, huku wengine wakipiga makofi, mbinja zikirindima kutoka huko na huko.

    KHAH!

    Brey akabaki akikodoa macho kwa kutoamini kile alichokuwa akikiona, kwani sasa yule dada alikuwa akitabasamu kwa furaha huku akimtazama moja kwa moja usoni huku akiendelea kucheza ile dansi ya aina yake.

    “BICHEI! Bichei!” Binti sasa alikuwa akilirudia tena lile neno.

    Zidadu akamshika Brey mkono, akamvuta.

    “Tuondoke hap…”

    Lakini hapo dada kichaa alichomoka mbele na kumng’angania Brey kwa nguvu mwilini.

    “No! Bichei! BICHEIII…BICHEI HII, HII, HIIII…!” Alipayuka kwa kelele za wazimu wa wazi, na Brey akajihisi akiishiwa nguvu na hapo hapo akili ikamuingia kiza…akashindwa kufikiri wala kuamua. Zidadu alimpiga ngwara kali yule dada, watu wakaachia miguno ya fadhaa wakati dada akigaragara hovyo ardhini, naye akamvuta Brey kimabavu kutoka eneo lile. Binti akainuka na kuzidi kupiga kelele, sasa akilia kwa uchungu huku akimnyooshea kidole Brey.

    “Bicheiii…Bicheiiii…ooo Bichei, jamani….!”

    LAH!

    Zidadu alifanikiwa kumfikisha Brey garini kwao na kuliondoa kutoka eneo lile kwa kasi sana.

    “Ni nini kilichokea pale, Zidadu?” Brey alimuuliza mdhibiti wake kwa mashaka makubwa.

    “Shit, mimi ndio nikuulize wewe ni nini kilichotokea pale! Kwa nini ulizubaa namna ile pale wewe? Hadi chizi anakufikia na kukung’ang’ania namna ile? What’s the matter with you, gaddemit?” Zidadu alimjia juu.

    “Ah…sijui…yule dada…? Bichei? Nini yote ile…?” Brey alizidi kuuliza huku akijiuliza. Zidadu akasonya na kuzidisha kasi.

    “Yule kichaa alinitambua Zidadu...ananijua kutokea wapi? Na kwa nini analinasibisha lile neno bishei…”

    “Bichei!” Zidadu alimrekebisha kwa ukali.

    “hilo hilo…! Kwa nini analinasibisha na mimi?”

    “Sijui na sidhani kama ni hivyo…ni kichaa yule!”

    “Na amenitambua, pamoja na uchizi wake…we ulisema huku hakuna atakayenitambua!” Brey alifoka na kupiga ngumi ndani ya kiganja cha mkono wake kwa hasira.

    “Sidhani kama ni hivyo…yule ni chizi na mwenyewe umeona!”

    “Kwa hiyo katika gulio lote lile akaona aunadi uchizi wake kwangu? Siamini hilo hata kidogo…the girl has to die!” Brey alifoka, akimalizia kauli yake kwa azimio kuwa ni lazima yule dada auawe.





    Zidadu hakumjibu lolote muda ule. Aliendelea kuendesha gari akiwa kimya, uso akiwa ameukunja kwa tafakuri. Brey naye akaamua kupiga kimya, akijikita kwenye kusugua ubongo juu ya kile kilichomtokea kule gulioni.

    Ni nani yule dada?

    Kwa nini aliniganda miye kati ya wote waliokuwepo pale na lile neno lake la kijinga?

    Na ile dansi aliyokuwa akicheza…? Mbona kama…?

    Mlipuko mkali wa maumivu ukamkita kichwani, akafumba macho kwa kubana maumivu yake huku akiuma meno na akigeukia pembeni. Moyo ukaanza kumuenda mbio. Alijiegemeza kitini akiwa amefumba macho namna ile huku akipigwa upepo uliotokana na mwendo wa gari lile. Kwa namna fulani akili ilimgomea kabisa kufanya kazi.

    Ilikuwa kama iliyoingia kiza…



    _______________



    "Na sasa unaweza kunielimisha ni kwa nini yule dada afe, Brey?" Zidadu alimuuliza, wakiwa wameshafika nyumbani kwao, na Brey akiwa amaeshatulia na kikombe cha chai ya rangi mkononi. Zidadu alikuwa anapiga Heineken aipendayo sana.

    "Kwa nini asife? Sitaki kubahatisha usalama wa maisha yangu mimi..." Alijibiwa, naye akatikisa kichwa kwa masikitiko.

    "Na umakini wako uko wapi sasa wewe? Badala ya kusema tumbane na kuweza kuelewa anakujua kutokea wapi… unataka tumuue?" Alimuuliza, na Brey akafyatua ulimi kwa kukereka.

    "Zidadu....unambana chizi ili akueleze nini? Angekuwa mtu mwenye akili zake hakika ningetaka sana kumbana na kumhoji ananijua from where...lakini chizi? Chizi hatuelezi lolote zaidi ya kutuamshia tu udadisi kutoka kwa watu...shit, kuniamshia mimi udadisi kutoka kwa watu!" Brey alimjia juu mdhibiti wake.

    Zidadu alimtazama kwa muda, kisha akashusha pumzi ndefu.

    "Nilihofia sana kuwa tulikuwa tunatengenza “killing machine” wakati tunakupa mafunzo ya mambo haya, Brey...na sasa naona ndicho tulichobakiwa nacho...mashine ya mauaji tu." Alisema kwa simanzi kidogo, na Brey akatikisa kichwa.

    "Si siku nyingi sana nilikusikia ukisena kuwa unajivunia kuwa sehemu ya walioshiriki kunifanya niwe hivi...leo unaongea vinginevyo?" Alimuuliza kwa kushutumu.

    "Hapana Brey...tulikufunza kuua kwa kujihami na kwa kulitumikia taifa lako...sio kwa kujifurahisha tu! Yote uliyoyafanya huko nyuma kabla ya leo ninajivunia nayo sana…maana yamewezesha kutimia kwa lile ambalo wengi miongoni mwa watu na mataifa wamelishindwa…"

    "Sasa kwani nimekwambia nataka chizi afe kwa kujifurahisha nafsi tu? Hii ni mimi kujihami nafsi yangu Zidadu! Mi nataka niishi kama raia wengine sasa… nitumie pesa zangu bwana...haya maisha ya kila niendako lazima nigeuke nyuma siyapendi! Sikuwahi kuyapenda asilani! Chizi wako anataka kunirudisha huko...so n’tamuua ili kuyahami maisha yangu ya baadae!" Brey alijitetea kwa jazba, lakini Zidadu alishaanza kumtikisia kichwa kumbishia kabla hata hajamaliza utetezi wake.

    "Bado nasisitiza chizi afuatiliwe kwanza...huenda isiwe kwenye maslahi yako kumuua..." Alimwambia.

    "Meaning what?" Brey alihoji kwa komombo, akimaanisha anataka Zidadu amueleweshe alikuwa anamaanisha nini kwa kauli yake ile.

    "Kama mara mbili wakati tunakabiliana na yule chizi nilikuona ukimtazama kwa namna isiyoeleweka Brey...na ndio maana hata umakini ukatupotea kiasi ukaruhusu aweze kukung'ang'ania mwilini kama alivyofanya...Brey tuliyemfunza sisi mbinu za medani asingeruhusu hilo asilani!"

    Khah?

    Brey akaduwaa.

    Machoni akadhihirisha kuwa ile ilikuwa ni habari mpya kabisa kwake. Zidadu akaliona hilo machoni mwake.

    "Ndio maana nasisitiza tena kuwa chizi mcheza ngoma inabidi afuatiliwe....tujue kuna nini kati yake na wewe...”

    “Kati yangu nay eye…?”

    “Of Course! Kwani picha niliyoiona pale inaniambia kuwa kuna kitu kati yako..." Zidadu alimjibu na kuweka kituo, kisha akaendelea huku akimtomasa kwa kidole chake kifuani, "...na wewe!"

    Brey akaduwaa.

    “Sasa kama ni hivyo…si wewe ndiye ungetakiwa ujue? Si ni wewe ndiye unayetakiwa unieleze kila kitu kuhusu maisha yangu ya awali ambayo hata mimi najishangaa kuwa siyakumbuki?”

    “Hili si miongoni mwa niyajuayo Brey…”

    “Kwa nini? Ni nani ajuaye sasa?”

    “Ukweli ni kwamba sidhani kama kuna ajuaye kila kitu...kila mtu aliyehusishwa na wewe alikujua kuanzia pale tu alipokutanishwa nawe…mimi nilikutanishwa nawe kwenye mafunzo, tena sehemu tu ya mafunzo, kabla hujapotea kwa miaka…hatimaye nikaja kuambiwa kuwa unarudi tena kwangu kukuongoza kwenye maisha yako ya uraiani…sijui kila kitu Brey.” Zidadu alisema.

    “Sasa…dah! Mi’ nilishakuwa radhi kuendelea kuwa mimi nijijuaye hivi sasa…lakini sasa, nalazimika kujitafuta ili nijijue nilikuwa nani huko kabla...nahitaji kumbukumbu zangu aisee…” Alisema.

    “Na ndio moja ya sababu ya mimi kuwa nawe katika kipindi hiki. Ili hatimaye niseme kuwa Brey Jabba sasa anaweza kuachwa akaishi uraiani bila kuwa madhara kwake na kwa jamii inayomzunguka...sasa hili la leo linanipa ugumu sana kuthibitisha hilo. Huwezi kuua tu kila unayemhisi anahatarisha maisha yako, Brey…hauko tena kwenye operesheni sasa…uko uraiani sasa wewe…” Zidadu alimwambia.

    Brey Jabba akaishia kujishangaa.

    “Kwa hiyo, ukijiridhisha kuwa nitakuwa tishio kwa jamii ndio utakaponiua siyo?”

    “Siyo lengo, lakini ni moja kati ya hatua zitakazotakiwa kuchukuliwa…na mimi nataka kuhakikisha kuwa hatufiki huko. Nataka kuhakikisha kuwa Brey anapasi mtihani wa kuweza kusihi uraiani bila ya kuwa na athari za kazi aliyotumwa na taifa kuifanya...kazi iliyomkutanisha na watu na matukio ya kutisha, kazi iliyomhalalishia kuua kwa kadiri alivyoona inafaa ili kutimiza jukumu lake, bila kuchukuliwa hatua yoyote…lakini sasa jukumu limeisha na umeshalipwa jaza yako…inabidi nihakikishe unakuwa mtu salama kubaki uraiani.” Zidadu alitoa hotuba.

    Brey akapiga kimya kirefu sana, na Zidadu hakumharakisha. Hatimaye aliinua uso wake na kumtazmaa moja kwa moja Zidadu usoni.

    “Okay… tumfuatilie huyu chini Zidadu…na tuchimbe undani wa maisha yake…labdo humo ndani tutaweza kunikuta na mimi nikiwemo…okay?” Alimwambia.

    “Okay, hapo sasa unaingea vilivyo ndivyo…” Zidadu alisema.

    “Na kitu kimoja lazima nikukumbushe mzee…” Brey alimwambia akiwa makini sana, na Zidadu akamuinulia kope kuashiria kuwa liakuwa anamsikiliza. “Usidhani utaweza kuniua kibwege…kama itafikia hatua hiyo basi jua kuwa nitapapambana nawe ka uwezo wangu wote!”

    Zidadu akacheka.

    “Amini usiamini Brey…hatutafikia huko, ila kama tukifika huko, basi itakuwa haki sawa…niytakupa nafasi ya kukjitetea ile aidha nife mii au ufe wewe…ila nikifa mimi, jua kuna wengine watakaokufuata…na dip utakaporudi kwenye yale yale maisha ya kutemnea huku ukigeuka geuka nyuma. Hutaki kuishi maisha hayo Brey. Tushuirukiane ili uvuke mtihani huu…nibaki kuwa mjomba wako tu.” Yalikuwa ni maneno mazito. Na kwa hakika yalimuingia vizuroi sana Brey.

    “Okay mjomba.,..tumsake chizi sasa…”

    “Indeed!”

    “Tunaanzaje?”

    “Mi narudi teha kule gulioni…na nitafuatilia kuanzia pale…”

    “Tunaenda wote…”

    “Halafu akikuona aanze tena yale mayenu ya Bichei? NO way…wacha nikachunguze…halafu nikijua anapopatikania, tunamuibukia bila ya kuw ana kadamnasi ya watu…”

    “Dah, kwa hiyo mi nikae tu hapa kama kiwete?”

    “Tafuta la kufanya..tazama muvi, soma vitabu, kapaliliea bustani huko nje…wacha mi nikafuatulie hili swala…” Zidadu alimjibu, na Brey akacheka kwa huzuni.

    Dakika kumi baadaye Brey alikuwa akimtazama yule bwana waliyekubaliana kuwa aendelee kuwa mjomba wake, akiwa amevaa kanzu na barghashia iliyochakaa, na akiwa amebandika miwani ya kusomea usoni na mkongojo mkononi. Akajikuta akitabasamu.

    “Hivi nitaonekana tofauti na nilivyokuwa kule gulioni hapo awali…” Zidadu alisema huku akiingia kwenye ile Toyota Stout yake na kuondoka kurudi kule sokoni.



    _____________



    Haikumchukua muda Zidadu kupata habari za yule dada kichaa mara aliporudi kule gulioni, kwani bado alikuta mazungumzo ya kile kituko yakiendelea. Alidodosa zaidi na kidogo kidogo akapata yale aliyokuwa anayataka. Dada kichaa na mama yake walikuwa wanaishi kijiji cha tatu kutoka kwenye kile cha kwao. Na walikuwa wamekuja pale kijijini kipindi kile kumfuata mganga maarufu wa kienyeji, ambaye waliamini kuwa angeweza kumtibu yule dada mwenye sura ya kuvutia. Zidadu hakuishia hapo. Akataka kujua jina la huyo mganga, kwani hata yeye alikuwa ana kijana wake ambaye alikuwa amelemaa miguu ghafla tu, na amehangaika sana.

    Hapo tena akapata zaidi.

    Wachuuzi wa pale gulioni aliokuwa akiwadodosa wakamtajia waganga zaidi ya sita watakaoweza kumsaidia tatizo lake.

    “Dah wallahi nashukuru…je na huyo ambaye huyo dada kichaa mnayemsema amekuja kumuona? Ni nani huyo?” Alihoji zaidi, akionesha kumakinika sana na ile habari.

    “Oh, huyo ni mzee Tupa huyo…kiboko ya wachawi…kijiji chote hiki anaogopeka!” Alijibiwa.

    Zidadu akashukuru na kuondoka. Alipofika mbele akaanza kuulizia ni wapi atakapompata mganga mashuhuri aitwaye mzee Tupa. Hakuuliza sana. Kijana mmoja alijitolea kumpeleka kabisa hadi kwa huyo mzee.

    Akiwa ameegesha gari lake mbali kidogo na gulio, akajitolea kulipia baiskeli mbili za kukodi, na akapelekwa hadi kwa huyo mganga.

    Na huko akakutana na mama Gisla…









    Aliingia ndani ya uwa wa nyumba ya tofali ya yule mzee aliyeelekezwa kuwa ndiye mzee Tupa na kuwa ndiye ambaye yule dada kichaa alipelekwa kwake ili kupata tiba. Japo nyumba ile ilikuwa imejengwa kwa matofali na kuezekwa kwa mabati ya kawaida yaliyochoka, haikuwa imepigwa plasta na ule uwa wake ulikuwa ni wa matete.

    Ndani ya wigo wa nyumba ile alikuta akina mama watatu wakiwa wamekaa kwenye mkeka...na mmoja wao alikuwa ni yule mama aliyekuwa akimkamata yule dada kichaa kule gulioni saa chache tu zilizopita.

    Aliwasalimu...wakamutikia. Akaulizia kuonana na mzee Tupa.

    Mmoja wa wale akina mama ambaye alijinadi kuwa ni mke wa mzee Tupa akamjuza kuwa kwa muda ule alikuwa anamhudmia mgonjwa mwingine mle ndani...na kwamba akitoka huyo anayehudumiwa alikuwa anaingia yule mama mwingine aliyekuwa ameketi pale mkekani na yule mama aliyemuona kule gulioni asubuhi ile.

    "La Haula! Kwa hiyo akitoka na huyo tena anaigia na huyu ndio na miye nisikilizwe?" Zidadu aliyeonekana mzee kuliko umri wake kwa mavazi aliyovaa alijitia kuuliza kwa hamaniko huku akimuoneshea yule mama aliyemuona kule gulioni asubuhi ile.

    "Hapana...mwanaye huyo ndio anayehudumiwa hivi sasa...ina maana akitoka huyu mama mwingine hapa unaweza kuingia na wewe mzee wangu..." Mke wa mzee Tupa akamtoa mashaka.

    "Oh afadhali...naweza kusubiri basi..." Zidadu alijisemesha huku akizungusha macho huku na huko, akitafuta pa kukaa. Mke wa mganga akainuka na kumkabidhi kigoda.

    "Karibu kigoda basi usubiri baba..."

    "Ooh ahsante...ahsante sana mama..." Zidadu alikipokea kile kigoda kisha akakiweka karibu kabisa na yule mama wa yule kichaa aliyeambiwa kuwa alikuwa anatibiwa humo ndani.

    Akaanza kujiongelesha jinsi gani tatizo la kijana wake lilivyokuwa kubwa...na hata hajui kama kuna aliyekumbwa na tatizo kubwa namna ile hapa duniani. Yule mama aliyekaa karibu yake akaguna.

    "Usiseme hivyo baba…ungesikia matatizo ya wengine sidhani kama ungesema hivyo...wako wenye mazito kuliko hayo yaliyomkuta kijana wako..." Alimwambia kwa simanzi nzito.

    "Mnh...inawezekana kweli? La kwangu ni zito sana mama...yaani kijana katoka asubuhi anatembea, mchana napigiwa simu kuwa ameaguka njiani miguu haifanyi kazi!! Hapana hili ni zito sana kwa kweli!" Zidadu alijiongelesha kiuongo.

    Yule mama alimtazama na kuguna, kisha akageukia pembeni huku akimjibu.

    "Sasa ungejua yalomkuta Gisla wangu je?”

    Zidadu akawa ameshalipata jina la yule binti ncheza ngoma gulioni.

    “La bintiyo laweza kuwa zito kwa upande wako mama, sikatai hilo…ila hili langu! Mnnh!” Alimjibu.

    “Sasa mi binti yangu ametoka mchana kwenda kwenye mazoezi ya kucheza hii miziki yao vijana wa siku hizi...anarudi nyumbani kama saa tatu baadaye akiwa amerukwa akili!" Mama akampasulia la kwake.

    "Eeenh??" Zidadu akajikuta akishangaa kiukweli, akiwa ametumbua macho.

    "Yaani hivi hivi tu??" Akasaili zaidi.

    "Kabisa babaangu...kisa nini? Milioni tano tu!" Mama alijibu, na Zidadu akazidisha umakini.

    "Sijaelewa mama…kwamba kapata wazimu kisa milioni tano kivipi...? Aliiba wakamroga...au...?"

    "Si bora angeiba? Tungesema karogwa kwa jambo alilotenda...wala hakuiba mwanangu...alirogwa tu ili asisinde hayo mashindano...yaani ni ujinga mkubwa kabisa kwa kweli. Sasa sijui wamepata wao hizo milioni tano hata sielewi!" Mama alisema kwa simanzi.

    Zidadu akamakinika zaidi.

    "Heh! Hilo mbona balaa...ni lini mambo haya mamaangu?" Alihoji zaidi.

    Mama akafyatua cheko ya huzuni

    "Hata sina hakika tena babaangu...nadhani ni mwaka wa tano huu sasa..."

    Ama!

    Akili ikamchemka Zidadu...alijaribu kuunga mahesabu ya miaka.

    "Eh! Sasa...Lah! Ina maana miaka yote hiyo...ndio leo unamleta kwa mtaalamu?"

    Mama Gisla akatikisa kichwa kwa simanzi.

    "Baba nimehangaika mimi! Si Kusi wala si Kasi...si juu wala si chini...kote nimezunguka. Miaka na miaka...mtoto haponi. Nimeenda mahospitalini na kwa waganga kadhaa wa kadhaa...lakini wapi...mpaka nilipofika hapa ndio kidogo nikaanza kuona dalili..."

    "Ah...kumbe ulishakuwa hapa kwa muda eenh?"

    Nina wiki nzima hapa...na alishaanza kupata unafuu fulani...hadi leo nikasema tukatembee kidogo huko gulioni...” Mama alisema na kupiga makofi kwa kukata tamaa, “Si vikacharuka upya...? Tena vibaya sana..." Akaanza kuangusha machozi.

    "Basi mamaangu...pole sana. Natumai atapona tu ili mrudi nyumbani...si mnaishi hapa hapa kijijini eenh?" Zidadu alisema kwa huzuni iliyoendana na mazingira aliyokuwa nayo yule mama...na hapo hapo akatupa swali lake la mtego.

    "Ahsante...na hapana...sisi hatuishi kijiji hiki..." Mama alimjibu huku akijifuta machozi kwa khanga, kisha akamtajia kijiji walichokuwa wanatoka.

    Yes!

    Zidadu alishangilia kimoyo moyo.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Dah, kweli lako zito mama…pole sana!”

    Mama alimuitika kwa kichwa tu huku akilia, na hapo ukelele mkubwa ukasikika kutokea kule ndani.

    “BICHEEEEEEEIIIIII, BICHEI…BICH…BICHH..EE..E..IIIIIII!!”

    “Ohooo!” Mama alimaka huku akiinuka na kukimbilia kule ndani bila hata kuitwa.

    Zidadu alitikisa kichwa kwa masikitiko mazito.

    Zilisikika sauti za kukemeana huko ndani, mayowe kati ya binti na sauti nyigine ya kiume ya kiutu uzima, na sauti ya yule mama akilia huku akijaribu kumuongelesha yule bintiye. Mke wa Mganga naye akainuka na kuingia ndani. Taratibu Zidadu akajiinua na kuondoka zake.



    _________________



    Ilikuwa ni saa tisa alasiri wakati alipoingia tena kule nyumbani kwao, na kufikia muda huo Brey Jabba alikuwa ameshajaa upepo vibaya sana. Alishampigia simu mara kadhaa lakini ile simu haikuwa hewani.

    “Nini kimekuchukua masaa yote hayo Zidadu? Na kwa nini hukuwa ukipatikana simuni?” Alimhoji kwa wahka mara alipongia mle ndani.

    Badala ya kumjibu, Zidadu alienda moja kwa moja hadi kwenye jokofu, akatoa Heineken baridi na kupitiliza nayo hadi kwenye kochi akajibwaga na kutundika miguu yake juu ya meza iliyokuwa pale sebuleni, akapiga “tarumbeta” refu kwa chupa ile, akisajili picha ya kutatanisha kwa yale mavazi aliyovaa na kile kinywaji alichokuwa anakigida muda ule.

    “Nakuuliza swali Zidadu…!” Brey alimfuata pale akiwa amejazbika vilivyo.

    “Maswali, sio swali.” Zidadu alimrekebisha, kisha akapiga funda jingine fupi la kile kinywaji.

    “It doesn’t matter, bwana! Nipe majibu basi…nini kimetokea huko… umegundua nini?”

    “Unakumbuka mtu aitwaye Gisla?” Zidadu alimtupia swali huku akimtazama kwa makini, na Brey hakuonesha kukumbuka lolote kuhusu jina hilo.

    “No! Sina jina hilo kwenye kumbukumbu zangu…ni nani huyo?”

    “Una hakika Brey?” Zidadu alimuuliza akiwa hana utani hata kidogo.

    “Of Course nina hakika…who the hell is that person, eenh” Brey alimjia juu akisisitiza kwa kimombo kuwa aelezwe huyo Gisla ni nani.

    “Ndio kichaa wako huyo…” Zidadu alimjibu huku akimtazama.

    Brey akakunja uso.

    “Ndio jina lake?” Alimuuliza.

    “Yap…!”

    “Kwa hiyo imekuchukua muda wote huu…karibu siku nzima, kwenda kugundua jina lake tu?” Brey alimjia juu, na Zidadu akapiga funda jingine kubwa la kile kinywaji chake kisha akaibamiza mezani ile chupa ikiw atupu naye akiinuka.

    “Wewe na yule binti mnajuana Brey…”

    “Whaat?”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ndio! Sasa binti angekuwa timamu angenifahamisha mnajuana vipi…lakin ndio hivyo tena…kadata. Aliye timamu kati yenu ninyi wawili hizi sasa ni wewe tu hapa. Sasa naomba uniambie…unamjua vipi yule binti?” Zidadu alimkabili huku akimtazama moja kwa moja machoni.

    Brey akamtumbulia macho kwa hasira.

    “Simjui yule binti…na silikumbuki hilo jina…”

    “Mnajuana Brey.”

    Halikuwa swali.

    Brey akamkasirikia.

    “Fafanua basi Zidadu…mi sikuelewi ujue!”

    Zidadu akamsimulia mtiririko wa maongezi yake na yule mama aliyemkuta pale kwa mganga mzee Tupa. Alipomaliza bado Brey akawa hajaelewa.

    “Riwaya ya kusikitisha sana hiyo…lakini bado sioni inahusika vipi na mimi. Na iweje hiyo riwaya ikuaminishe kuwa mimi ninajuana na huyo dada aliyerogwa?” Alimuuliza.

    Ndipo Zidadu alipotoa picha iliyochakaa kutoka mfukoni kwake na kumkabidhi.

    “Hebu jaribu kuunganisha hiyo uliyoiita riwaya, na hii picha hapa…halafu uniambie kuwa hakuna uhusiano kati yako na yule crazy dancer kule!” Alimwambia, na Brey akainyakua haraka ile picha.

    Akaitazama. Mdomo ukamuanguka. Macho yakamtumbuka yakiwa kwenye ile picha. Na yalipoinuka kumtazama tena Zidadu, yale macho yalikuwa yamechanganyikiwa kwa utovu wa uelewa…







    _______________



    Sehemu nyingine ya kijiji mzee Tupa mganga wa kienyeji alikuwa akitazamwa kwa macho yaliyojawa utovu wa uelewa kama alivyokuwa akizamwa Zidadu muda ule…ila yeye alikuwa akitazamwa namna ile na mama Gisla.

    “Sasa mimi nitampata wapi huyo mtu lakini baba?” Mama Gisla alimuuliza huku akiwa anakipapasa kichwa cha bintiye kilicholala mapajani mwake huku yule bintiye akiwa ametopea kwenye usingizi mzito baada ya kunusishwa unga fulani na yule mganga.

    Mzee Tupa alimung’unya midomo kwa namna ambayo wateja wake wengi walikuwa wameshaiona.

    “Ni muhimu huyo mtu aliyesababisha huyu binti alipuke kwa namna unavyonielezea na kurudia kweye hali hii nimuone…yumkini kuna kitu kinachohusiana na tatizo lake…”

    “Sasa pale ni sokoni mzee wangu, na wala sikuweza kumtilia maanani huyo mtu…” Mama alilalamika.

    “Lakini si umesema ilikuwa wazi kabisa kuwa binti alimtambua yule mtu?” Mzee Tupa akasaili.

    “Ni kweli hilo baba lakini…”

    “Na wakati hapo kabla hata wewe tu mama yake alikuwa hakutambui?”

    “Ndio mzee wangu…”

    “Na alikuwa haongei kabisa?”

    “Kimya moja kwa moja baba! Kazi kucheza madansi hovyo tu mitaani, na hata hivyo…ni kimya kimya tu!” Mama alimjibu kwa kuchanganyikiwa.

    “Huyo mtu ana mzimu ndani yake…mzimu ulioweza kumuamsha huyu mgonjwa wangu…namtaka! Nitamsaka....!” Mzee Tupa alisema na kuazimia.

    “Lini sasa babaangu?” Mama Gisla akasaili kwa wahka.

    “Nilitaka kujua tu kama wewe utakuwa unamfahamu au utaweza kumkumbuka…bahati mbaya ndio humfahamu wala humkumbuki…” Mzee Tupa alisema huku akimumng’unya midomo yake kiasi yule mama alifanya bidii sana kumsikiliza kwa makini ili amuelewe.

    “Simjui kabisa yule mtu…lakini mimi ni mgeni hapa kijijini kwenu…pale gulioni wako wengi waliomuona…huenda ukiulizia utaweza kumgundua!” Mama alitoa rai.

    “Si neno…nitaongea na mizimu yangu…iisake mizimu ya huyo rijali aliyeishika mizimu ya binti yako!” Mzee Tupa alisema na kuishia kuunguruma kwa muda mrefu mithili ya simba, macho yakiwa yamemtumbuka na povu likimtoka kinywani.

    Mama wa watu akaishia kulia kwa uchungu tu.



    ______________



    “Huyu si ndiye yule dada wa kule gulioni leo hii huyu?” Kule nyumbani kwake, Brey alikuwa anauliza, bado utovu wa uelewa ukiwa umemsheheni machoni.

    “Ndiye huyo…” Zidadu alimthibitishia.

    “Na…na…na huyu aliyezungushiwa duara jekundu usoni…?” Brey aliuliza tena kwa kitetemeshi dhahiri, na hapo Zidadu akafyatua cheko fupi. Akaenda na kuichukua tena ile picha kutoka mikononi mwa Brey na kuitazama upya.

    “Hilo my dear Brey…” Alisema huku akiitazama ile picha ambayo sasa ilikuwa mkononi mwake, kisha akamuinulia Brey uso wake na kumalizia, “…ndilo ninalotaka wewe ujaribu kunielewesha…”

    Aka!

    Brey akaketi kochini bila kujua kuwa alikuwa ameketi, taswira ya picha iliyokuwa mkononi mwa Zidadu muda ule ikiwa imejigongelea vizuri sana akilini mwake.

    Ilikuwa ni picha iliyomuonesha yule dada aliyekutana naye kule gulioni asubuhi ile, lakini akiwa binti mdogo zaidi ya vile alivyomuona asubuhi ile, akiwa katika hatua mojawapo ya kucheza dansi, au ngoma, jukwaani. Alikuwa ameitazama moja kwa moja kamera huku akiwa ameachia tabasamu mororo sana lililoonesha kuwa alikuwa akifurahia kile alichokuwa akikifanya wakati ule. Kando ya yule binti alikuwa kijana mwingine wa kiume ambaye bila shaka alikuwa akicheza ile ngoma au dansi pamoja na yule dada, kiasi akionekana kama kwamba walikuwa wakicheza kwa hatua za kufanana, lakini binti alikuwa ameinua mguu wa kulia na jamaa alikuwa ameinua mguu wa kushoto. Wote wakionekana kufurahia sana ile ngoma au dansi waliyokuwa wakiicheza. Kwa namna fulani akili ya Brey ilimtuma kuwa kuna kitu hakikuwa sawa kwenye ile picha…kwenye zile hatua za dansi zilizonaswa na kamera. Alidhani kama wote yule binti na yule kijana aliyekuwa akicheza naye wangekuwa wameinua juu miguu yao ya kulia ndio ingekuwa sawasawa.

    Ni wazi lililopita haraka sana kichwani mwake, kisha likapotea. Akamtazama kwa muda yule jamaa aliyekuwa akicheza na yule binti pale pichani. Lakini huyu siye ambaye sura yake ilikuwa imezungushiwa duara kwa kalamu nyekundu. Siye ambaye Brey alitaka kujua kutoka kwa Zidadu kuwa ni nani na kwa nini sura yake ilikuwa imezungushiwa lile duara jekundu. Na siye ambaye sasa Zidadu alikuwa anamtaka yeye ajaribu kumuelewesha kuwa ni nani.

    Akahamishia macho yake kwenye sura iliyozungushiwa duara jekundu pale pichani. Koo likamkauka, ingawa akili yake haikuwa imegubikwa kiza tena.

    “Umeipataje hii picha wewe…I mean umeipata wapi…kwa yule dada kichaa?” Alimuuliza kwa sauti ya kukwaruza, bado utovu wa uelewa ukiwa wazi machoni mwake.

    “Hujajibu swali langu Brey Jabba the killing machine…lakini nadhani sasa unaona kuwa maisha sio kuua watu tu, eenh? Basi nitakupa muda zaidi wa kulitafakari hilo swali langu…”

    “Sihitaji kutafakari nahitaji jibu Zidadu!” Brey alifoka.

    Zidadu alimtazama kwa muda, akapandisha na kushusa pumzi ndefu. Akaenda kuketi karibu na pale alipokuwa, akamtazama usoni.

    “Nitakueleza nimeipataje hiyo picha, na nikishamaliza nitataka unifahamishe juu ya huyo jamaa aliyezungushiwa duara jekundu hapo…sawa?” Alimwambia, na Brey akamtunishia midomo kwa hasira, wala hakujishughulisha kumjibu.

    Na Zidadu akaguna.

    “Uliniuliza kuwa nimetumia muda wote nilioutumia kule gulioni kwa kulijua jina la yule crazy dancer tu…nikakujibu sivyo. Sasa nilikuwa wapi muda mwingine wote huo?” Alianza maelezo yake.

    Bado Brey hakumjibu zaidi ya kumrushia miale ya moto kwa macho yake.

    Bila kuzijali zile ghadhabu zake, Zidadu akamueleza…



    _______________



    Alitoka pale nyumbani kwa mzee Tupa mganga wa kienyeji akiwa na vitu viwili muhimu kichwani mwake…jina la yule kichaa mcheza ngoma, na kijiji alichotokea.

    Moja kwa moja alirudi kwa baiskeli yake ya kukodi hadi kule gulioni alipoikodi na kuirudisha kwe mwenyewe. Kisha akalirudia gari lake na kuelekea kwenye kile kijiji walichotokea yule mama na bintiye mwenye wazimu. Alipofika kule kijijini, akiwa na uelewa wa uhakika kabisa kuwa yule binti kichaa alikuwa maarufu sana kutokana na utofauti wa wazimu wake, aliegeshja gari lake chini ya mti mmoja pale kijijini na kujichanganya kijijini.

    Akaenda kwenye duka ambalo lilionekana kuwa ni kubwa pale kijijini, hivyo karibu kila mkaazi alikuwa ana uhakika wa kufika kwenye duka lile. Akanunua vitu kadhaa vidogo vidogo kisha akamuuliza muuza duka ni wapi nyumbani kwa mama Gisla.

    “Oh, mama kichaa?” Muuza duka aliuliza huku akicheka.

    “Ndivyo mnavyomuita kumbe? Ndiye huyo huyo…ana binti yake mwenye athari ya akili hivi kidogo…” Zidadu alimjibu muuza duka. Jamaa akaangua kicheko kikubwa.

    “Athari ya akili kidogo? Wee bwana vipi? Yule ni mwehu wa kutupwa kabisa yule? Mi huwa nasema kila siku…zile ni bangi tu, watu wanabisha. Binti si alikuwa mcheza dansi yule? Atakuwa kakutana na mibangi tu huko kwenye vikundi vyao vya madansi na matokeo yake ndio hayo!” Jamaa alimwambia.

    “Ni mpwa wangu yule ujue…” Zidadu alimtishia , na jamaa akaachia mdomo wazi, yeye akaendelea haraka, “…sikuwa kijijini hapa kwa muda mrefu sana ndio maana nimeshindwa hata kukumbuka nyumbani kwa dadaang…”

    “Oooh samahani sana mzee, samahani sana...dah, si unajua tena? Ngoja nikuelekeze mzee wangu….” Jamaa alimjibu kwa kuhamanika.

    Na ndivyo Zidadu alivyoelekezwa nyumbani kwa akina Gisla.

    Akaenda hadi kwenye nyumba aliyoelekezwa ambayo nayo ilikuwa imezungushiwa uzio wa matete. Alibisha hodi kwa sauti, ingawa nyumba yenyewe tu ilimuambia kuwa hakukuwa na mtu mle ndani.

    Ina maana binti anaishi na mama yake tu yule, hana baba?

    Alijiuliza huku akiangaza huku na huko, kisha akazunguka nyuma kulikokuwa kuna banda la kuku na zizi la mbuzi. Kutokea kule nyuma hakupata taabu kuingia ndani ya nyumba ile iliyokuwa ikinuka upweke. Alipekuwa vyumba viwili vya mle ndani akitumia tochi ya simu yake ya mkononi, maana pamoja na kwamba muda haukuwa usiku bado mle ndani kulikuwa kuna kiza. Chumba cha kwanza alikuta dalili kuwa ndicho kilichokuwa kikitumika kwa malazi. Chumba cha pili hakikuwa na dalili yoyote ya kutumika kwa muda mrefu.

    Alimakinika zaidi na kile chumba cha pili. Akakipekuwa kwa makini lakini kwa uharaka wa kujiamini. Alikuta madaftari ya shule ya muda mrefu sana, sare za shule za zamani sana, za kike, na baadhi ya nguo za kawaida nazo za kike. Mapicha ya wanamuziki wa zamani wa nchi za magharibi yalikuwa yamekaukia sehemu kadhaa za kuta za chumba kile. Akapekuwa zaidi, akakutana na albamu ya picha. Akaketi kitandani na kuipekuwa kwa makini zaidi ile albamu.

    Ndipo alipokutana na ile picha iliyomshitua sana moyo wake…



    _______________



    Brey alimtumbulia macho kwa kutoamini baada ya kusikia namna alivyoweza kuipata ile picha.

    “Sasa umeshajua niliipataje hiyo picha Brey…je uko tayari kunijibu kuhusu huyo mtu aliyezungushiwa duara jekundu hapo pichani?” Zidadu alimuuliza huku akiitomasa kwa kidole chake cha shahada ile sura iliyokuwa imezungushiwa duara kwenye ile picha.

    Brey alikohoa kidogo, akamtazama kwa macho yenye mashaka.

    “Mimi siku zote nimekuwa nikiamini kuwa sina ndugu hapa duniani…kumbe inaweza kuwa nina ndugu…?” Alisema kwa mashaka, na kabla hata hajamaliza Zidadu alikuwa ameshaanza kumtikisia kichwa kumkatalia.

    “Iangalie vizuri hiyo picha Brey…” Alimwambia.

    Na Brey akaitazama ile sura ya kijana aliyekuwa amesimama nyuma ya wale wawili walioonekana wakicheza dansi au ngoma kwenye ile picha. Yule kijana aliyezungushiwa duara alikuwa miongoni mwa waliokuwa wakitazama ile ngoma au dansi iliyokuwa ikichezwa na wale wawili, wao wakiwa nyuma ya jukwaa, na huyu ambaye alikuwa amezungushiwa lile duara alikuwa amekenua meno kwa kuchekelea huku ameinua juu mikono yake akipiga makofi.

    Ni kwamba Brey Jabba alikuwa akijitazama yeye mwenyewe kama alivyokuwa miaka kadhaa nyuma…naye kipindi ile picha inapigwa alikuwa bado barobaro tu, kama jinsi yule dada wa gulioni alivyoonekana kuwa alikuwa ni binti ndogo tu pale pichani.

    Tatizo hakuwa na kumbukumbu yoyote ya tukio lile maishani mwake.

    “Huyo ni wewe Brey…na ndio maana nikasema kuwa wewe na yule dada mnajuana…mna historia ninyi wawili…”

    Sauti ya Zidadu ilimvumia masikioni, na Brey akachanganyikiwa zaidi.

    “Sio nduguyo huyo…sitaki kuamini mambo ya kwenye sinema za kihindi za Mithun wa shamba na Mithun wa mjini aisee...huyo ni wewe. Wewe na crazy dancer mna historia. Na historia hiyo ni kali sana kiasi cha yule kichaa kuweza kukutambua mara tu alipokuona pale gulioni leo hii.” Zidadu alizidi kumwambia.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mchomo mkali wa maumivu ukampasua kichwani Brey, na kiza kikamtanda sio akilini, bali mbele ya macho yake.

    “No! Sina kumbukumbu yoyote Zidadu…”Alimaka kwa hamaniko.

    “Na bado unataka kichaa wako auawe?” Zidadu alimuuliza.

    Brey akahamanika. Hakautoa jibu, badala yake akamtupia swali.

    “Sasa…ndio uliizungushia hili duara jekundu hii sura hapa ili iweje? Nisikose kuiona mara utakaponipatia hii picha…?”

    Zidadu alimtazama kwa muda.

    “Siye mimi niliyeizungushia hilo duara jekundu hiyo sura yako ya ujanani hapo Brey…nimeikuta hiyo picha ikiwa hivyo hivyo na hilo duara.”

    “Ati?”

    “Yes, Brey…

    Brey alichoka.

    “Sasa nakuuliza tena Brey Jabba the killing machine…bado unataka tukamuue kichaa wako?” Zidadu alimuuliza tena, na safari hii Brey hakusita.

    “Of course!”

    Mdomo ukamuanguka Zidadu Mgina…





    MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Blog