Search This Blog

Monday 24 October 2022

NI ZAMU YAKO KUFA - 4

 

    Simulizi : Ni Zamu Yako Kufa

    Sehemu Ya Nne (4)







    Jacob kwa kujua kuwa alikuwa anakabiliana na watu walio wajuzi katika kazi yao hii, hakuhitaji papara wala haraka ya mambo. Alikimbia kuelekea upande wa kushoto wa hoteli hiyo, huku mkono wake wa kushoto ukiwa unatoa bastola tayari kwa lolote. Aliingia ndani ya hoteli kwa kupitia mlango wa nyuma.

    Dakika moja baadae alikuwa jirani kabisa na kilipokuwa chumba chake alichokuwa amekodi mchana uliopita. Alisubiri hapo ili kuona kama kuna mtu angekuja. Hakuona mtu yeyote.

    Alienda mpaka jirani na kilipokuwa chumba cha Merina hapo alisimama kwa muda, lakini pia hakuona mtu yeyote akija wala kutoka ndani ya chumba hicho. Hakuwa na hakika kama Merina alikuwa ndani ya chumba hicho na wala hakutaka kuingia na kumshitua. Hivyo kwa haraka na njia ya panya Jacob alitembea na kujikuta tena yuko pale nje alipokuwa amesimama awali.

    Alipotupia macho ilipokuwa gari ya yule mama nadhifu, hakuiona. Mara moja akajua kuwa atakuwa amewapoteza tena. Walikuwa wameshaondoka.

    Wakati huu sasa Jacob akaona ni muda muafaka wa kumpigia simu Merina ili kujua pale alipo. Merina alipopokea alimtaarifu Jacob kuwa yuko chumbani, na kuwa hakuwa amepata usingizi bali alikuwa akimsubiri kwa muda wote. Jacob naye alimtaarifu kuwa alikuwa njiani kuelekea pale hotelini. Hakujua ni kwa nini aliamua kumdanganya.

    Tofauti na alivyomwambia Merina, mpelelezi Jacob Matata hakuelekea chumbani kwa Merina badala yake aliingia ndani ya gari na kuitia moto. Aliingia barabara na kuanza safari ya kuelekea mjini.

    Kwa mara nyingine safari yake iliishia Paradise hoteli. Hapo aliomba chumba cha kulala. Alijikuta ameamua kufanya hivyo makusudi. Mara nyingine Jacob aliamini kuwa katika kazi zao za ukachero hautakiwi mara zote kufanya unavyopanga kwani mipango yako yaweza kuwa mikononi mwa adui na ukaumia. Kubadilika badilika ni jambo la muhimu sana katika mchezo huu.

    Baada ya kukabidhiwa chumba 53, kuoga na kupata chakula alicholetewa na muhudumu chumbani hapo aliingia kitandani. Tayari ilikuwa saa tisa usiku.



    * * *



    Mlio wa simu ndiyo uliomwamsha Jacob. Aliichukua simu hiyo na kuangalia namba za mpigaji, zilionyesha kuwa aliyepiga ni Merina.

    “Hallow mrembo umeamka salama? Jacob alisabahi

    “Ndio ukafanya nini, kuniweka usiku kucha nikisubiri, au ulipita mwingine nini? Aliuliza kwa sauti ya utani.
    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Lilitokea jambo ambalo ilinilazimu nimalizane nalo, ila usijali maana sifi leo wala kesho ila usije ukanichoka tu” Jacob alisema katika hali ya utani pia

    “sasa tukutane wapi kwa ajili ya mipango mingine? Aliuliza huku akiwa anaamka toka kitandani.

    “Mimi nakuja hapo ulipo ili tupange” Merina alijibu

    “Hapa ni nje kabisa ya mji haitakuwa sehemu nzuri” Jacob aliongopa

    “nisubiri nakuja ili tujue leo tutanzia wapi” aliongeza na kukata simu.

    Baada ya kumaliza kuongea na Merina alienda kuoga na kisha akajiandaa kwa kutoka. Mara hii aliivaa sura nyingine ya bandia tofauti na ile aliyokuwa nayo jana. Alipohakikisha yuko katika hali aliyokuwa anaitaka na kuwa na kila kitu anachokitaka, alifunga mlango wa chumba na kuanza kuelekea nje. Alipitia mapokezi ambapo alilipa fedha kwa ajili ya malazi ya siku kumi. Aliamua kufanya hivyo makusudi kabisa.

    Dakika chache baadaye Jacob alikuwa anatambaza gari katika moja ya barabara nzuri za mji wa Arusha. Alikuwa Anaelekea Moivalo hoteli, hoteli ambayo Merina alikuwa amelala. Hoteli hii iko mbali toka Paradise hoteli, hoteli ambayo yeye Jacob alikuwa amelala usiku huo bila taarifa kwa yeyote.

    Alipofika Moivalo hoteli aliangalia hali ya usalama katika eneo hilo, baada ya kulidhishwa na hali ilivyo, kwanza alipanda mpaka chumbani kwake. Maana wote wawili yeye na Merina walikuwa wamechukua vyumba katika hoteli hii.

    Alipoingia chumbani kwake hakupata shida kubaini kuwa hapakuwa kama alivyokuwa amepaacha. Japo mtu au watu walioingia walijitahidi kutoacha alama yoyote ya kuonyesha kuwa mliwahi kuwa na mtu tofauti na yeye. Aliangalia sehemu zake za siri na kutambua kuwa wapekuaji walikuwa hawajafanikiwa kufika. Toka sehemu yake hiyo ya siri, alichukua baadhi ya vitu alivyoamini kuwa vingeweza kumsaidia kwa siku hiyo.

    Baada ya kuona kuwa amekamilika hakuona sababu ya kuendelea kuwamo katika chumba hicho kwani siku hiyo aliiona ni ya muhimu sana kwake.

    Alitoka chumbani kwake na kuelekea upande kulipokuwa chumba cha Merina. Mwili wake na akili ya Jacob vilikuwa katika hadhali kubwa. Alipokaribia chumba cha Merina aliangalia pande zote kuona kama kuna mtu aliyekuwa anasubiri uwepo wake mahali hapo. Eneo lote halikuwa na mtu hata mmoja, hivyo alifikia mlango wa chumba cha Merina na kuugonga. “Karibu mwana mpotevu” sauti ya Merina ilisikika ikisema.

    “Siyo yeye” Jacob alisema

    “Karibu ndani Jacob, mwana mpotevu” Alirudia mara hii kama mtu aliyekuwa anainuka. Jacob alinyonga kitasa cha mlango na kujikuta yuko ndani. Alipoingia ndani macho yake yalielekezwa moja kwa moja kitandani ambapo Merina alikuwa amekaa. Macho yake yalipogongana na ya Merina aliona kitu fulani kikipita katika mboni za macho ya Merina, ambacho hakuelewa ni nini. Merina aligeuzia macho kwenye kochi lililokuwa chumbani humo, Jacob alimwelewa kuwa alikuwa anataka nini hivyo alienda kukaa kwenye hilo kochi. Jacob alitambua nini maana yake, akakaa. Jacob alipokaa tu, Merina alitabasamu, tabasamu ambalo lilikuwa zuri lakini Jacob hakulipenda, sababu hasa ya kulichukia hakujua. “Ulijuaje kuwa ni mimi na wala si mhudumu? Jacob alimtupia swali Merina.

    “Nimesikia nyayo zako nikatambua” Alisema huku akichezeachezea nywele zake.

    “Unataka kuniambia kwa muda huu mfupi tu umeshakariri namna vishindo vya nyayo zangu vilivyo?

    “Kwa mtu kama wewe uliyeingia kwa ghafula moyoni mwangu si rahisi nishindwe kukariri vitu vidogo vidogo kama hivyo” Merina alisema huku macho yake yakionyesha hali ya ungavu wenye mvuto na aibu ya kike.

    Kwani kwa mila za kiafrika haijazoeleka kwa mwanamke kuanza kuelezea hisia zake za mapenzi kwa mwanamume. Mwanamke anaweza kuelezea kwa vitendo na si kwa maneno kama hivi anavyofanya Merina. Kama angepatikana aliyeanzisha utaratibu huo ingepaswa aulizwe kwamba ana uhakika gani kuwa mara zote mvulana ndiyo huwa wa kwanza kumpenda msichana? Kama yeyote anaweza kuanza kupenda kwa nini yeyote asiwe na uwezo wa kujieleza kwa mwenzie?

    “ Vipi kuna hatua yoyote uliyopiga katika kazi hii? Sauti ya Merina ilimzindua Jacob toka katika mawazo yake hayo.

    “Hakuna la haja”Alijibu huku macho yake yakiwa yanazunguka katika chumba hicho.

    Kuna jambo moja lisilo la kawaida ambalo Jacob aligundua ndani ya chumba hcho cha Merinai. Pamoja na maneno yote ya utani waliyokuwa wakitaniana na Merina lakini kuna harufu ya manukato ambayo Jacob alikuwa na hakika kuwa hayakuwa ya Merina, yalikuwa yakinukia katika chumba hiki. Hapo akajua kuwa muda mfupi tu uliopita kuliwahi kuwa na mtu katika chumba hicho tofauti na Merina.

    Lakini Merina mwenyewe alishamwambia Jacob kuwa kwa sasa hakutaka kujulikana na mtu yeyote kuwa yuko Arusha. Sasa ni nani huyo aliyekuwa amekuja na kuacha marashi hayo ndani ya chumba hicho? Jambo jingine ni kuwa Merina hakuwa ameshajiremba hivyo marashi haya hayakuwa yake.Ya nani sasa? Jacob alitaka kumwuliza lakini wazo jingine lilimpinga.

    Una hakika gani kuwa mtu aliyetumia marashi hayo hakuwa muhudumu tu wa hoteli? Wazo lilimpinga. Jambo jingine ni kuwa Merina angeweza kumwona kuwa ameanza kuwa na wivu sana juu yake jambo ambalo yeye Jacob hakutaka litokee.

    Wakati anafikiria hayo, Merina alikuwa ameshainuka na kuelekea bafuni kwa ajili ya kujiswafi. Vyumba vya hoteli hiyo vilikuwa ni vya kisasa kabisa, ilikuwa ni chumba na bafu lake. seti TV, computa iliyounganishwa kwenye mtandao, radio, friza na simu ya mezani ni baadhi ya vitu vilivyokipamba chumba hicho.

    Hivyo Merina alipoenda bafuni kuoga Jacob alibaki peke yake hapo chumbani. Dakika chache mara baada ya Merina kuwa ameingia bafuni, mara simu yake ya mkononi iliyokuwa juu ya kitanda ilianza kuita. Kwa vile sauti ya mlio wake ilikuwa ni ndogo haikuweza kumfikia huko bafuni. Hivyo iliendelea kuita kwa muda.

    Mwishowe simu hiyo ikawa kero kwa Jacob, alisimama na kuiendea. Aliichukua na kuangalia namba za mpigaji. Macho yalimtoka pima alipoiona jina la mpigaji. Hakuamini taarifa iliyokuwa ikiletwa na macho yake toka kwenye simu hiyo, kwani jina la mpigaji lilisomeka ‘Ndevu nyeupe’.

    Kweli hakutegemea kukutana na jina kama hilo kwenye simu ya mtu kama Merina, huku akijua fika kuwa mtu huyu tayari alikuwa ameshatuma taarifa nyingi za vitisho kuwajia. Mtu huyu anayejiita ‘Bosi mwenye ndevu nyeupe’ ndiye ambaye Jacob anashuku kuwa ndiye kiongozi wa kundi lililohusika na uingizwaji wa silaha za majaribio, vitisho vya mauaji ya viongozi na mauaji ya jaji Mark Gordon na mzee Edson ukiachilia mbali wengine wengi. Sasa imekuwaje Merina ahifadhi jina kama hilo katika simu yake? Maswali haya yote Jacob alijiuliza ndani ya muda mfupi tu, huku simu ikiendelea kuita. Alitaka ampelekee bafuni lakini alisita, alitaka kumwita lakini akaona haingekuwa vizuri pia. Mara vishindo vya Merina kuwa anatoka bafuni vikakasikia, tayari alikuwa ameshamaliza kuogaa.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Haraka Jacob aliirudisha hiyo simu mahali ilipokuwa mwanzo. Wakati Merina alipogusa kitasa cha mlango wa kutokea bafuni simu iliacha kulia. Bila shaka mpigaji alikuwa ameazimia kukata baada ya kugundua kuwa aliyempigia hakuwa jirani na simu.

    Merina aliingia huku akiwa amejifunga taulo na khanga moja tu, hilo halikuonyesha kumpa wasiwasi wowote. Alipofika jirani na ilipokuwa kabati ya nguo aligeuka na kumuangalia Jacob huku tabasamu lake la kutatanisha likiwa usoni. “Samahani kwa kukuchelewesha” hatimaye alisema huku akianza kuuandaa mwili wake.

    Kidogo Jacob aliingiwa na aibu baada ya kuona Merina ameanza kuvaa huku yeye akiwa amekaa hapo chumbani. “Ngoja nikupishe mamaa usije shindwa vaa vizuri, ila kuna mtu alikupigia pindi ukiwa bafuni, hivyo ni vema ukamshughulikia kwanza kabla hujaendele na shughuli” Jacob alisema hivyo makusudi ili aweze kuona Merina angeweza kuonyesha hali gani pindi akiiona ile namba ya mpigaji.

    Macho ya Jacob hayakumpa nafasi hata kidogo, yalikuwa sambamba na uso wake. Merina aliacha shughuli aliyokuwa anafanya na kuiendea ile simu pale kitandani. Alipoinyanyua na kuangalia namba ya mtu aliyekuwa amempigia ghafula uso wake ulibadilika. Alimwangalia Jacob huku akitabasamu kujaribu kuficha mshituko aliokuwa nao.

    ‘ Eeh bibie ni bwana ako nini mbona umefurahi kiasi hicho? Jacob alijifanya kuuliza “ mwambie kwa sasa huna nafasi kwa kuwa uko na mimi” Jacob aliongeza huku akiachia pozi ambalo ni kwa nadra sana huwa analionyesha kwa mtu.

    Merina hakujibu kitu badala yake alimwangali Jacob kwa macho ambayo yalikuwa na kila dalili ya kuudadisi uso wake. Alitaka kujua kama Jacob alikuwa na habari yoyote kutoka katika simu hiyo.

    Iliichukua ile simu na kuipeleka puani, kuangalia kama angegundua harufu ya marashi tofauti na yake. Mara moja Jacob akajua kuwa Merina alikuwa na mambo ambayo alitaka yeye asiyajue.

    Hakugundua harufu yoyote tofauti na marashi yake. Hakujua kuwa kwa maadili ya kipelelezi haitakiwi mpelelezi kujipulizia marashi. Labda iwe kwa sababu maalumu tu. Maana marashi yanaweza kufanya mtu aingie mikononi mwa adui yako haraka hasa nyakati ambazo huwa wanacheza na mauti kama mtoto anavyochezea mwanasesere wake. Hivyo Jacob Matata kwa kuzingatia hilo huwa hatumii marashi anapokuwa kazini.





    Alipohakikisha kuwa Jacob hakuwa ameshika simu hiyo kwa vile haikuwa na marashi tofauti na yake, Merina alisimama nayo na kurudi pale Kabatini. Japo alijitahidi kuficha mshituko alioupata mara baada ya kuiona namba hiyo ya ‘bosi mwenye ndevu nyeupe’ lakini hakufanikiwa mbele ya macho yaliyoenda shule ya kuchunguza kama ya Jacob.

    “Jacob simu hii imenirudisha mbali sana kifikra” alianza kusema huku akiendelea na kazi ya kujipodoa. Jacob hakuona tena haja ya kutoka nje ili ampishe avae, maana aliona wakati huo ulikuwa muhimu sana kuweza kumchunguza binti huyu ambaye sasa alikuwa ameanza kumuwekea alama za kuuliza.

    “Wapi huko bibie? Jacob alihoji kwa udadisi “kumbe aliyepiga ni tofauti na vile nilivyodhani mimi kuwa ni bwana yako? aliongeza.

    “Hapana huyu jamaa alikuwa ni rafiki mkubwa wa baba yangu. Tangu kifo cha baba yangu amekuwa akinisumbua mara kwa mara kuwa niende kuishi naye” Merina alisema huku mara hii macho yake yakiwa yameacha kuangalia kioo kilichokuwa mbele ya Kabati na badala yake yalituama usoni kwa Jacob. Kwa vile alikuwa na hakika kuwa Jacob alikuwa hajui lolote juu ya mpigaji wa simu, hivyo uso wake haukuonyesha wasiwasi wowote.

    “Kwani yeye anaishi wapi? Jacob alijitia mjinga na kuuliza zaidi huku akijifanya kutengeneza tai yake. Hakutaka Merina ajue kuwa maongezi yale yalikuwa na umuhimu mkubwa.

    “Anaishi Denmark, naye ni jaji kama alivyokuwa baba yangu, walisoma pamoja” Alisema huku akichukua begi lake lililokuwa na jozi kadhaa za viatu.

    “Kama umechunguza na kugundua kuwa anaweza kuishi na wewe kwa nini unamkatalia? Jacob alihoji

    “Sijamkatalia, ila sioni kama ni wakati muhafaka wa mimi kuchukua uamuzi wowote. Maamuzi kama hayo nitayafanya mara baada ya kuhitimisha hii kazi” alionge sentesi hiyo huku akiwa anamalizia kuvaa viatu.

    “Haya dada hayo ni maamuzi yako, lakini mara baada ya kasheshe hii hapa Arusha ningependa uondoke na mimi niwe wako uwe wangu. Lakini kama ulivyosema kuwa hayo yote utayafanyia maamuzi wakati ukishamaliza kazi hii iliyoko mbele yetu ya kuwasaka maharamia hawa wasio na roho ya kibinadamu. Lakini si vibaya nikisema mapema ili uanze kufikiria kuwa nataka ubaki na mimi”. Jacob alisema hayo huku akiwa anasimama kwa vile Merina pia alionyesha kuwa alikuwa tayari. Tofauti na Jacob aliyekuwa amebadilisha sura leo, yeye Merina alivaa sura ileile ya bandia aliyokuwa amevaa jana.

    “mwenzio leo bado sijanywa chai, lengo langu ni kupata chai nikiwa na wewe” Merina alisema hayo huku mkono wa Jacob tayari ulikuwa umeshakifikia kitasa cha mlango. “Ombi lako limekubaliwa ila…” kabla hajamalizia Jacob alikatizwa na busu toka kwa Merina ambaye alikuwa ameshajisogeza karibu kabisa na yeye.

    “Asante” Jacob alisema huku akimwangalia Merina usoni. Macho yao yalipogongana kwa karibu kiasi hicho Merina alitaka kufanya kitu, lakini Jacob akamkatisha. “Hayo yatafanyika baada ya kazi kwani marehemu mzee Edson na baba yako jaji Mark Gordon wakituona tunafanya hivi ili hali watu waliowaondoa duniani kwa nguvu wakiwa hawajashughulikiwa, wanaweza kutulaumu sana. Hivyo ni vema tukatafuta ni nini tunaweza kufanya ili kusogea karibu zaidi na watu hawa hatari na katili” Merina aliposikia hayo hakuwa na la kusema zaidi ya kuchukua funguo za chumba hicho toka kwenye pochi lake na kuufunga mlango nyuma yao.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ukweli ni kuwa mpaka wakati huo Jacob hakumchukulia Merina kama mshirika wake tena, badala yake alimwona kama mtu anayestahili kuchunguzwa.

    Walitoka nje na kuongoza moja kwa moja mpaka pale Jacob alipokuwa ameegesha gari yake. Jacob hakupenda kuwa wa kwanza kuingia, hivyo alimwashiria Merina aanze kuingia ndani ya gari. Alifanya hivyo makusudi kwani kanzia hapo alikuwa ameadhimia kuanza kufuatilia kila nyendo ya binti huyo. Alipohakikisha kuwa hakukuwa na lolote jipya mahali hapo, naye aliingia ndani ya gari.

    “Ulikuwa umepanga tukapate kifungua kinywa katika hoteli gani? Jacob alimwuliza Merina alipokuwa tayari ameshawasha gari tayari kwa kuondoka.

    “Serengeti hoteli, pale huwa wanapika supu nzuri ya mbuzi” alijibu huku akitengeneza nywele zake.

    Jacob hakumjibu chochote, badala yake aliondoa gari. Alipita mitaa kadhaa akiendesha, huku wote wakiwa kimya. Kichwani Jacob alijua fika kuwa ilimbidi afanye juu chini mpaka apate nyendo za yule ‘mzee mwenye kipara’ na ‘mama nadhifu’. Alihisi kuwa hawa ni watu wa karibu sana na huyu mtu anayejiita ‘bosi mwenye ndevu nyeupe’.

    “Merina, itabidi leo tuzungukie kenye kumbi mbalimbali za starehe ili tuweza kupata angalau mtu mmoja kati ya wale ambao tayari tumeshawashuku tangu tuanze kazi hii. Tutakuwa tumepiga hatua kubwa sana kama tutafanikiwa kumpata yule ‘mzee mwenye kipara’. Huyu tunaweza kumlazimisha akatupa habari zinazoweza kutusaidia kuingia ndani ya kundi hili hatari” Jacob alisema hayo huku akimwangalia Merina kupitia kioo cha mbele cha gari. Merina alitingisha kichwa kuashiria kukubaliana na yale yalisemwa.

    Tofauti na alivyokuwa amependekeza Merina, Jacob alikuwa akilizungusha gari katika mitaa pasipo kuonyesha dalili yoyote ya kuelekea Serengeti hoteli. Alifanya hivyo makusudi kabisa. Jambo moja lililomshangaza ni kuwa Merina akushitushwa wala hakumwuliza ni kwa nini alikuwa akifanya hivyo, badala yake muda mwingi alionekana kutabasamu tu.

    Baada ya kuzunguka kwa muda, hatimaye Jacob aliegesha gari Green Valley jirani na makao makuu ya Polisi mkoa wa Arusha. Hapo ndipo alipouona mshangao wa Merina. Kwanza alionekana kukasirika kwa kile kitendo cha Jacob kutokwenda sehemu aliyokuwa amependekeza wakapate kifungua kinywa asubuhi hiyo. Hapo napo hakusema kitu huku akijaribu kuficha hali yake ya kuchukia, hakujua kuwa Jacob alikuwa tayari ameshausoma uso wake kupitia kwenye kioo cha mbele cha gari.

    “Samahani bibie nimekumbuka kuwa kuna mtu nina miadi naye mahali hapa, hivyo nimeona itakuwa ni vizuri tukawa tunamsubiri ili hali tunapata kifungua kinywa. Hii haimaanishi kuwa nimedharau maoni yako, la hasha, ila ni katika jitihada za kufanikisha maongezi yetu” Jacob aliongopa hivyo mara baada ya kuwa ameegesha gari katika sehemu ya maegesho Green Valley. “Sawa mzee maadamu unaona kuwa uamuzi huu utakuwa na manufaa katika harakati yetu hii sina la kupinga. Tukae upand….” Kabla Merina hajamaliza kauli yake ilikatizwa na mlio wa simu yake ya mkononi. Kwanza alionyesha kushituka, lakini kama kawaida yake alificha mshituko huo kwa tabasamu tamu huku akimwangalia Jacob usoni.

    “Nadhani hutajali kama nitaongelea pembeni? Alisema

    “bila shaka, mototo mzuri kama wewe unahitaji kuwa na uhuru na usiri wa mambo unayodhani usingependa wengine tujue” Jacob alijibu, lakini moyo wake ulikuwa na hamu ya kusikiliza maongezi hayo. Merina alisogea pembeni umbali ambao kwa hakika isingekuwa rahisi kusikia kilichokuwa kikiongelewa kati yake na mpigaji wa simu ile. Kilichomfanya Jacob ahisi kuwa wenda simu ile haikuwa nzuri ni kitendo cha Merina kuwa anatupa jicho huku alikokuwa amekaaa kila baada ya muda mfupi. Jicho lenyewe lilionyesha dhahili kuwa alikuwa anataka ajue kama Jacob alikuwa anafuatilia au ametilia shaka maongezi hayo. Jacob hakuonyesha wasiwasi wowote, alikuwa anamwangalia kwa usiri mkubwa. Alipomaliza kuongea na ile simu, alirudi pale kwenye gari.

    “Samahani kwa kukuweka kwa muda mrefu” alisema huku akimpigapiga Jacob mgongoni .

    “Ungependa tukae wapi wakati tukipata kifungua kinywa? Jacob aliuliza huku akiwa anafunga milango ya gari.

    “Kona ile pale naona imetulia sana” Merina alionyesha huku akianza kutembea. Kwa hadhali kubwa Jacob aliongozana naye mapaka pale alipukuwa amepachagua. Baada ya kuwa wameshakaa, kila mmoja aliagiza aina ya kifungua kinywa ambacho alikuwa akipendelea. Maongezi ya hapa na pale yaliendelea mpaka pale muhudumu alipowaletea vitu walivyokuwa wameagiza. Walianza kupata kifungua kinywa huku Merina akionekana kushamiri katika maongezi.

    “Samahani, naenda maliwatoni mara moja” Jacob alisema huku akiinuka na kuanza kuelekea maliwato. Alipoingia kwenye korido iliyokuwa ikielekea sehemu kulipokuwa na vyoo, alitembea kwa haraka zaidi. Alipofika mbele hakuingia maliwato, badala yake alichepuka kushoto na kushika korido nyingine. Hiyo ilimchukua mpaka ulipo mlango wa upande mwingine wa hoteli hii. Alipofika mlangoni aliangalia kulia na kushoto, alikiona alichokuwa akikitaka. Alitoka na kuelekea upande wa kushoto ambapo kulikuwa na taxi.

    “Nipeleke Serengeti hoteli haraka iwezekanavyo” Jacob alimwamuru dereva aliyekuwa anajisomea gazeti.

    “Ok, ni shilingi elfu tano tu kakangu”

    “Sawa” Alisema huku tayari akiwa ameshaingia ndani ya gari na kukaa viti vya nyuma.

    “Unapendelea muziki gani? Dereva aliuliza akimaanisha kuwa alikuwa akitaka kumwekea kanda kama kiburudisho kwa mteja wake.

    “Ukimya na kufikiri sana ndiyo muziki naoupendelea zaidi kuliko yote” Jacob alisema jibu lilionekana kumshangaza huyo jamaa. Hivyo hakuweka kanda yoyote.

    Dakika mbili baadaye walikuwa wameshafikia lango kuu la kuingilia Serengeti hoteli. “Naomba uniache hapa panatosha” Jacob alisema huku akiwa anamkabidhi ujira wake. Wakati dereva huyo anakumbuka kusema asante tayari Jacob alikuwa ameshatoka nje.

    Aliamua kuja hapa kuangalia kama kuna yeyota aliyekuwa akisubiri kuwasili kwao, yeye na Merina katika hoteli hiyo ya Serengeti. Alihisi kuwa yawezekana chaguo la Merina kuja katika hoteli hiyo halikuwa la bure. Baada ya yule mwenye gari kuondoka Jacob alipapasa bastola yake na kuona iko sehemu iliyo tayari kwa kutumiwa. Badala ya kupitia mlango wa mbele wa hoteli hii, alitembea pembezoni mwa ukuta mpaka upande ambao kulikuwa na mlango wa kuingilia kwa nyuma. Hapo kabla ya kuingia, aliangalia pande zote kama kulikuwa na mtu aliyekuwa akifuatilia lolote. Kama paka aliyekuwa akipiga mahesabu ya kumnyatia panya, alianza kuingia ndani ya eneo hili la hoteli.

    Kulikuwa na eneo la kuegeshea magari upande wa kulia, upande wa kushoto kulikuwa na watu waliokuwa wamekaa chini ya miti mizuri hapo nje kabla hujaingia ndani. Jacob alitembea mpaka upande ule kulikokuwa na watu wamekaa wakijipatia yale yaliyokuwa yamewaleta mahali hapo. Alitafuta kiti akaketi katika hali ya geresha. http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Haikumchukua muda mrefu kuweza kumwona mtu aliyekuwa akitarajia kuwa wenda angekuwepo mahali hapa. Mtu mwenyewe alikuwa ni kijana mmoja aliyeonekana kuwa ni mtanashati wa haja. Alimwangalia kwa makini huku yeye akionekana kutomtambua kabisa Jacob. Jacob alisimama na kuanza kuelekea upande ule aliokuwa amesimama yule kijana ambaye alikuwa akivuta sigara. Jacob hakusita kutambua kuwa kijana huyo alikuwa akimsubiri mtu, tena mtu aliyekuwa akisubiriwa si kwa heri bali kwa shari. Jacob alitambua kuwa mtu aliyekuwa akisubiriwa ni yeye.

    Alikuwa amebakiza kama hatua sita hivi ili aweze kufika pale alipokuwa yule kijana. Mara simu ya kiganjani ya kijana huyo ilianza kuita. Jacob alipopiga hatua mbili zaidi kumkaribia, mara moja sura ya yule kijana ikawa imeshabadilika, yawezekana ni kutokana na yale aliyokuwa ameambiwa kwenye simu.

    Mara aliingiza mkono wake mfukoni kutaka kutoa bastola yake, hata hivyo hakufanikiwa kufanya hivyo kwani tayari bastola ya Jacob ilikuwa usoni ikisubiri kumpumulia. Aliinua macho kumtazama Jacob kwa hofu, lakini mara yaliangalia nyuma ya Jacob. Hapo Jacob akajua kuna kitu, hakusubiri kuambiwa, kwa staili ya aina yake tayari alikuwa amejirusha chini na kuviringika huku risasi zilizokuwa zimekusudiwa kumpata zikiwa zinamwingia yule kijana. Jacob aliendelea kuviringika huku akiangalia uwezekano wa kuweza kugeuka huku akiwa chini. Risasi ziliendelea kumiminika kila alipokuwa akitoka, kwa vile alikuwa anaviringika kwa staili ya kupindapinda adui alishindwa kumpata kwa shabaha yake.





    Jacob alipopata nafasi ya kusimama tayari alikuwa usawa wa ukuta. Risasi zilikoma, naye kwa kasi ya ajabu aliangaza macho huku na huko, hakufanikiwa kumwona adui, zaidi ya watu ambao sasa walikuwa wakikimbia hovyo katika eneo hilo la hoteli. Haraka alikimbia mpaka nje ya hoteli kwa upande wa barabarani, wakati anafika tu nje alisikia mlio wa gari ikiondolewa kwa kasi. Akaangalia kushoto na kulia, mara akamwona mzee mmoja ndiyo anataka kuingia ndani ya gari aina ya Range Rover Discover. Alikimbia mpaka pale alipokuwepo, alimpiga kofi moja kali la usoni kisha akamvutia ndani ya gari. Kwa jinsi alivyokuwa amempiga, ingemchukua mzee huyo si chini ya masaa manne ili aweze kurudiwa na fahamu. Alimweka kwenye siti za nyuma, kisha akaliondoa gari kwa kasi.

    Mambo yaliyofanyika hapo hayakuchukua zaidi ya dakika tano. Kila kitu kilifanyika kwa kasi na ufundi mkubwa. Haikuhitajika kupoteza hata dakika moja. Mwendo alioondoka nao ulifanya mataili yatoe moshi. Jacob alikuwa amefanikiwa kuona gari hilo lilipokuwa limeelekea, hivyo aliongeza mwendo kuelekea upande huo. Baada ya muda tayari akawa ameshaliona gari alilokuwa analifukuzia, badala ya kupunguza mwendo, aliongeza, ili aweze kulipita hilo gari. Gari ilikuwa imechukua mwelekeo kama inataka kutoka nje ya mji sasa ilikuwa karibu na maduka ya shoprite. Na kweli baada ya mwendo kidogo alikuwa sambamba na gari hilo, wakati analipita akapata nafasi ya kutupia macho ndani ya gari. Mtu aliyemwona ndani ya gari alimfanya atabasamu. Alikuwa ni yule mzee mwenye kipara, ambaye bila shaka ndio alikuwa kiongozi wa kufanya mauaji. Jacob aliipita gari hilo kwa kasi. Baada ya kulipita hakupunguza mwendo ili asimtie wasi wasi yule mzee mwenye kipara. Aliendelea mbele huku akiangalia nyuma asilipoteze hilo gari.

    Baada ya kuona amekuwa umbali wa kutosha toka lilipokuwa gari la mzee mwenye kipara, Jacob Matata alipunguza mwendo. Mbele kulikuwa na makutano ya barabara, Jacob aliingia barabara nyingine ambapo hakwenda mbele zaidi. Alisimama ili apate nafasi ya kuona kama yule mzee angeendelea au angekata hapo alipokuwa amekata. Mara ile gari ya mzee mwenye kipara ikampita katika mwendo mdogo. Naye akarudi katika barabara hiyo ambayo kwa sasa ilikuwa ni ile ya kuelekea monduli. Alikuwa akimfuatilia kwa taratibu wakati huu, hakuwa na haraka.

    Yule mzee aliendelea na mwendo wake wa taratibu mpaka alipofika mbele kabisa karibu na hoteli moja ya kitalii. Hapo alikata kushoto na kuingia kwenye barabara iliyokuwa ikielekea yalipokuwa makazi ya watu wenye uwezo. Badala ya kukata kama alivyokuwa amefanya yeye Jacob alipitiliza na kwenda kusimama kwa mbele, na kisha akasimamisha gari. Alishuka ndani ya gari na kusimamisha taxi moja iliyoonekana kutokuwa na abiria.

    “Naomba ufuate hiyo barabara” Alisema Jacob mara baada ya kuwa ameshaingia ndani taxi hiyo huku akimnyooshea kidole kuelekea kule alikokuwa ameelekea mzee mwenye kipara. Dereva huyo hakuuliza badala yake aligeuza gari na kuingia hiyo barabara.

    Jacob alitupa macho kwa mbele lakini hakuweza kuiona gari ya mzee mwenye kipara.

    “Tafadhali jitahidi kuongeza mwendo” Kauli hiyo ilimfanya dereva huyo aendeshe gari kama yuko mashindano ya magari. Baada ya mwendo kidogo waliweza kuiona tena ile gari ya mzee mwenye kipara, lakini safari hii ilikuwa ikiacha barabara na kuingia upande mwingine ambao ulionyesha kuwa kulikuwa na nyumba.

    “Hebu punguza mwendo nataka niangalie kitu fulani hapo” Jacob alisema huku macho yake yakiwa pima kuelekea kule ilipokuwa ikiingia gari ya mzee mwenye kipara. Hatimaye wao walikuwa wameshafika sehemu ile aliyokuwa ameingia yule mzee. Kwa vile dereva hakuwa anajua kitu gani kilikuwa kikiendelea, aliendelea na safari. Jacob alipoiona nyumba aliyokuwa ameingia mzee mwenye kipara hakuona sababu yakuendelea na safari.

    “Hivi unaweza kuendelea na njia hii kisha ukatokea mjini? Jacob alimwuliza

    “Hamna taabu lakini tunaweza chelewa kidogo maana itabidi turudi mpaka Sombetini kisha ndipo tushike barabara kuu ya Monduli ili kurudi mjini” Alisema huku akiongeza mwendo wa gari.



    * * *



    Saa sita kamili mchana ilimkuta mpelelezi Jacob Matata ameshafika Green Valley. Alimkuta Merina akiwa amekaa mahali palepale alipokuwa amemwacha wakati anaondoka kwenda Serengeti hoteli.

    “Ndio ukafanya nini, kidogo nianze kufikiri kuwa huenda nawe umeshapatwa na ‘bosi mwenye ndevu nyeupe’. Vipi salama lakini huko utokako? Alisema Merina huku macho yake yakijaribu kusoma uso wa Jacob.

    “Ndiyo, ila nina habari njema. Nilipoenda huko uani nilifanikiwa kumwona yule mzee mwenye kipara, ikabidi zianze kukuru kakala za kutafutana. Nimefanikiwa kumpata na nimemwoji lakini hakunipa habari nyingi kama nilivyotarajia. Hivi sasa ninavyoongea na wewe mzee mwenye kipara ni marehemu. Jacob alisema huku macho yake yakiwa sambamba na uso wa Merina. Aliamua kuongopa makusudi ili aweze kuona kama kweli Merina ndiye aliyekuwa amemshitua yule kijana pale alipokuwa ameenda Serengeti hoteli. Baada ya kusema kuwa mzee mwenye kipara ni marehemu, Jacob aliweza kuuona mshituko ulioushika uso na macho ya Merina, japo alijitahidi kuficha.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kwa taarifa nilizopata ni kuwa Bosi mwenye ndevu nyeupe ndiye mkuu wa kundi hili katika operesheni hii, lakini mkuu kabisa wa kikundi hiki anaitwa Mtakatifu wa kuzimu ambaye hakai hapa nchini. Wote wanaonekana kutumia majina ya bandia”. Jacob alitoa maelezo hayo yote ya kubuni katika hali ya kutaka kumpima Merina. Hata hivyo hakutaka kusema lolote juu ya mtu aitwaye malaika wa giza.

    “Kwa maana hiyo leo usiku natarajia kuwapata wengi wao pale Triple A club, maana nimeambiwa kuwa mara nyingi hupendelea kukaa hapo wakati wa usiku. Ni Lazima tujiandae kwa kazi ya usiku wa leo maana inaonekana watakuwa wengi na wakiwa wamejaa hasira kufuatia kifo cha yule mzee mwenye kipara” Jacob alisema.

    “Hapa sasa kazi itakuwa nzuri maana inaonyesha tumeshaanza kupata mlango wa kuingilia. Hizi sura za bandia tunazozitumia inaonyesha kuwa zinatusaidia sana. Mimi nafikiri mpaka kufikia kesho asubuhi tutakuwa tumeshapiga hatua kubwa sana katika kuwasaka hawa jamaa. Ni imani yangu kuwa tutafanikiwa kuvuruga mipango yao na kuweza kulisambaratisha kundi hili hatari” Marina alisema huku akiuvaa uso wa huzuni na hasira kwa wakati mmoja.

    Badaa ya maongezi na mipango mirefu ya kitakachofanyika usiku huo, waliamua kupata chakula cha mchana hapo hapo Green Valley hoteli. Walipomaliza kula waliagana kila mmoja akapate muda wa kupumzika, ili ifikapo saa mbili za usiku siku hiyo wote wakutane Triple A night Club.

    Lakini tofauti na makubaliano, Jacob hakwenda hotelini kupumzika kama walivyopatana na Merina. Alipotoka tu hapo Green Valley, alikwenda moja kwa moja mpaka Pradise hoteli. Hakuna aliyekuwa anafahamu kuwa Jacob alikuwa akiishi hapo kwani hata Merina alijua kuwa walikuwa wamechukua vyumba katika hoteli moja. Alipofika hapo Paradise Hoteli aliingia chumbani na kubadilisha sura kwa kuvua ile ya bandia akajibadilisha tena kidogo.

    Wakati saa nane kasoro dakika kadhaa mchana huo inaingia, Jacob alikuwa amefika jirani na taxi moja iliyokuwa imeegesha sehemu ya kuegeshea magari katika hoteli hiyo.

    “Naomba unipeleke Monduli mara moja” Alisema huku akiweka vizuri mkoba wake aliokuwa ameuchukua maalumu kwa safari hiyo. Ndani ya mkoba huo kulikuwa na kamera maalumu ya kipelelezi ambayo inaweza kuchukua picha katika mazingira yoyote. Pamoja nayo alichukua vitu vingine vingi alivyoamini kuwa vitamsaidia kule alikokuwa akielekea. Safari hii aliamua kwenda kufanya uchunguzi kwenye nyumba aliyoona mzee mwenye kipara anaingia.

    “Itakuwa shilingi elfu Ishirini tu”Alisema yule dereva huku akitia gari moto.

    “sawa twende” Jacob alijibu kwa sauti yabisi.

    “Naomba uniache hapa, ila kabla hujaondoka naomba uniachie namba yako ya simu ili pindi nitakapomaliza shughuli zangu nikupigie uje kunichukua” Jacob alisema mara baada ya kuona wamekaribia ile barabara iliyokuwa inaingia kwenye nyumba aliyokuwa ameingia mzee mwenye kipara. Hakutaka ashukie karibu sana na ilipokuwa nyumba hiyo. Alitoa simu yake ya mkononi na kuhifadhi namba za simu za yule dereva, kisha akimwacha aende wakati mwenye akianza kutembea kueleke upande ule wa ile nyumba.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nyumba aliyokuwa anaiendea ilikuwa mbali kidogo toka barabarani. Ilikuwa imezungukwa na msitu mkubwa wa miti. Alitembea mpaka alipokuwa amefika usawa wa nyumba hiyo, aligeuza kichwa kwa chati na kuangalia. Haikuwa rahisi kuona ndani kwani ilikuwa imezungushiwa ukuta mrefu sana, huku kwa mbele kukiwa na lango kubwa lililokuwa na langi ya bluu. Alionekana kama mpita njia wa kawaida tu, hakusimama wala kupunguza mwendo. Alipopita njia iliyokuwa inelekea nyumbani kwa mzee mwenye kipara, kwa mbele alikutana na kijinjia kingine. Akapinda na kuanza kukifuata maana kilikuwa kinaeleke upande uleule kulikokuwa na nyumba ya mzee mwenye kipara. Muda wote huu macho yake yalikuwa hayaachi kuangalia nyumba hiyo.

    Alipoangalia mwisho wa kijinjia hicho alichokuwa anapita sasa, akaona kuwa kingempeleka mpaka mtaa wa nyuma toka ule ilipokuwa nyumba ya mzee mwenye kipara. Hivyo akaona heri aende na kuona kama upande huo angepata mwanya mzuri wa kuichunguza nyumba hiyo. Kweli alipomaliza barabara hiyo alijikuta yuko mtaa mwingine, lakini hata hivyo aliweza kuiona nyumba ya mzee mwenye kipara.

    Kwa tahadhali na umakini mkubwa Jacob aliweza kujipenyeza kwenye vichochoro vya nyumba za jirani mpaka akawa ameufikia uzio wa nyumba hiyo kwa upande wa nyuma. Hapo aliangaza pande zote kuona kama kulikuwa na yeyote aliyemwona. Hali ilikuwa kimya kabisa, sana sana ndege walisikika wakiimba katika hali ya kumsifu mungu wao aliyewaepusha wasiishi na watu kama huyu mzee mwenye kipara.

    Alipohakikisha kuwa hakukuwa na matata yoyote, kwa mwendo wa kunyata alianza kuzunguka uzio wa jumba hilo. Alipofika mwisho wa ukuta huu kwa upande huu wa nyuma alichungulia ule upande mwingine. Upande huo ulikuwa wazi kiasi kuwa haukuwa salama sana.

    Ukuta ulikuwa ni mrefu kiasi kuwa haikuwa rahisi hata kuchungulia ndani. Jacob alifikiri kwa sekunde kadhaa nini cha kufanya. Hatimaye alipata jibu, alifungua ule mkoba wake aliokuwa ameubeba, humo alitoa ‘gloves’ za mkononi kisha akazivaa. Hizo zilikuwa maalumu kwa kuta ndefu kama huo uliokuwa mbele yake.Humwezesha mvaaji kupanda ukuta bila kuteleza anaposhika ukutani.

    Alichukua bastola yake na kuiweka mahali ambapo ingekuwa rahisi kuitoa na kuitumia kwa haraka. Alifunga vizuri mkoba wake na kuanza kuupanda huo ukuta. Alipofika kimo cha kuweza kuona ndani aliinua kichwa na kuchungulia ili kuona kama kulikuwa na mlinzi yeyote. Hapakuwa na mlinzi yeyote zaidi ya mijibwa mikubwa miwili. Mbwa hao walikuwa na kimo cha ndama, na walikuwa wakizunguka zunguka eneo hilo kwa ndani. Mkono mmoja aliendelea kushikilia ukuta na mkono mwingine alitumia kufungulia zipu ya mkoba wake. Humo alitoa dawa fulani kisha akaidondoshea kwa ndani. Muda mfupi baadaye wale mbwa walikuja upande ule, walipofika usawa aliokuwa Jacob walianza kuchezesha mikia yao. Tayari walikuwa wameshanusa harufu ya Jacob, japoa hakuwa amejipulizia marashi lakini Mbwa wana uwezo wa kusikia harufu kwa uwezo mkubwa. Kabla hata hawajaanza kupiga kelele walikuwa wameshafika kwenye zile dawa alizokuwa amedondoshea ndani. Wa kwanza alinusa na kutoka, mbwa wa pili kadhalika alifika na kuinusa ile dawa. Wakati wa pili ananusa yule wa kwanza aliyenusa mwanzo alianguka chini. Yule wa pili alipogeuka amwangalie mwenzake na yeye pia alianguka. Wote wakawa wameshapoteza fahamu. Lengo la Jacob likawa limetimia, zile dawa zilifanya kazi yake. Kwa umakini kabisa Jacob alitumbukia ndani bila kutoa kishindo.

    Alitembea upande huo, huku akijaribu kutega sikio kwenye dirisha alilokuwa akifika. Wakati anaikaribia kufika mwisho wa ukuta huo upande wa kushoto alipotega sikio kwenye dirisha lilokuwa hapo alisikia sauti ya mtu akiongea. Alitega sikio kwa ukaribu zaidi, alisikia sauti ikiongea huku msemaji akionekana kuwa amefurahia jambo maana alikuwa akicheka muda wote.

    “ Inaonekana una habari nzuri sana kuhusu huyo kichaa Jacob Matata, anasema ameniua, basi leo huko Triple A club anakosema ndiko atakwenda kuchukua kifo chake, awafuate hao anaojifanya kuwatetea. Tangu lini maiti akatetewa bwana. Naamini kuwa bosi mwenye ndevu nyeupe atafurahi sana kusikia taarifa za kifo cha Jacob. Maana anasema kuwa mtakatifu wa kuzimu amempa siku chache sana ili kuhakikisha kuwa Jacob Matata ameondolewa duniani. Kwa kifupi hatakiwi kutoka Arusha akiwa hai. Sasa unasikia malaika wa giza, hebu njoo hapa mara moja ili nikupe maagizo muhimu toka juu”. Ilisema sauti hiyo ambayo Jacob alihisi kuwa ni ya Max japo hakuwa na hakika sana maana ni miaka mingi imepita tangu mara ya mwisho walipoonana na Max.

    Jacob aliposikia maelezo hayo nywele zikamsimama. Sasa akawa ameanza kupata picha halisi, nayo ni kuwa Merina ni mshirika katika kundi hilo.

    Mara hii akaoanisha hali ya mambo na lile tukio ambapo aliiona namba ya bosi mwenye ndevu nyeupe ikiita kwenye simu ya Merina. Wakati akiwaza hayo mara alisikia muungurumo wa gari ikija. Alinyata mpaka akawa usawa wa kona ya ukuta. Hapo aliweza kuona mpaka mbele kabisa ambapo kulikuwa na lango kuu la kuingilia. Lango lilifunguliwa, gari ndogo aina ya RAV 4 iliingia. Jacob alitoa kamera yake tayari kwa kuchukua picha. Ndani ya gari alishuka binti mmoja mabaye Jacob hakuweza kumtambua. Kwa kamera yake alichukua picha kadhaa.

    Yule binti alipoanza kutembea, ndipo Jacob alipogundua kuwa hakuwa mwingine ila Merina. Alitembea kwa madaha kuelekea ndani. Kwa vile Jacob bado alikuwa karibu na kile chumba ambacho hapo awali alimsikia mzee mwenye kipara akiongea, mara hii tena alisikia sauti ikiongea tokea ndani. Sauti hiyo ilikuwa kana kwamba inaamuru “Waruhusuni wageni wangu wote wawili waingie” Mtu aliyeamuru aliposema hivyo aliangua kicheko cha kutisha. Alipomaliza kucheka tu mambo mawili yalitokea kwa wakati mmoja. Jacob alisikia kitu baridi kikigusa shingo yake, halafu ule ukuta aliokuwa ameegemea ukawa kana kwamba unaanguka. Ukuta huo ulipotelea aridhini. Kukawa na uwazi mkubwa. Jacob akajikuta anawataza walioko ndani bila kizuizi chochote. “Karibu ndani bwana Jacob Matata, japo sifurahii kukukaribisha katika mazingira kama haya, maana mimi si katili kiasi hicho” Wakati maneno hayo yakimtoka Max, mlango mwingine ulifunguliwa na Merina aliingia huku mikono akiwa ameweka juu. Ilikuwa wazi kuwa mambo hayakuwa shwari kwake pia.









    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog