Search This Blog

Thursday 27 October 2022

MUUAJI ASAKWE - 1

 







    IMEANDIKWA NA : PATRICK J. MASSAWE



    *********************************************************************************



    Simulizi : Muuaji Asakwe

    Sehemu Ya Kwanza (1)



    Utangulizi



    Mwanamke mrembo anauawa ndani ya bafu, nyumbani kwake, eneo la Tabata, Jijini Dar es Salaam. Kwanza kabisa, muuaji huyo katili alimtumia ujumbe wa vitisho muda mfupi tu kabla ya kutekeleza mauaji hayo. Pia, muuaji huyo alimbaka mrembo huyo kabla ya kumuua. Upelelezi wa Jeshi la Polisi, unafanyika mara moja. Msako mkali dhidi ya muuaji huyo unafanyika, na inagundulika siri nzito iliyojificha nyuma ya mapazia kuhusiana na kifo hicho chenye utata. Kama kawaida, mtunzi wako mahiri,  PATRICK J. MASSAWE anatiririka na hadithi hii ya kusisimua.     Fuatilia mpaka mwisho wake…



    MCHANA  wa saa sita hivi, John Bosho  alikuwa ndani ya gari lake aina ya Toyota Harrier  la rangi ya fedha, lililokuwa na kiyoyozi kilichompatia hewa nzuri ya ubaridi kiasi cha kulifukuza joto lililokuwa linafukuta huko nje.  Muda huo alikuwa anatafuta eneo la kupaki gari hilo, kwenye maegesho, nje ya Hoteli ya The Kibo II Anex, mtaa wa Kipata, eneo la Gerezani.



    Hii ni hoteli iliyopo ndani ya jumba la ghorofa tano, linalopakana kabisa na jengo la ghorofa, linalomilikiwa na Shirikisho la Vyama vya Ushirika, katika Barabara ya Lumumba, umbali wa mita tano hivi, na pia siyo mbali sana na Viwanja vya Mnazi Mmoja. Baada ya kulipaki gari hilo, John Bosho alishuka na hatimaye kuingia ndani ya hoteli hiyo maarufu yenye hadhi, ambayo alizoea kwenda mara kwa mara kujipatia chakula cha mchana.



    Kama kawaida, John Bosho alipoingia, alichagua meza moja ya pembeni na kukaa ili aweze kupatiwa huduma ya chakula. Kabla ya kuagiza chakula, aliangaza macho yake katika pembe zote za humo ndani, ambapo palikuwa na wateja kadhaa waliokuwa wanakula. Akiwa ni mwenyeji pale, aliweza kuhudumiwa chakula alichokipenda, aina ya wali kwa nyama ya ng’ombe.  Aliendelea kula taratibu huku akiangalia jinsi wateja wengine walivyokuwa wanaingia.



    Wakati John Bosho akiendelea kula chakula chake taratibu, mara akaingia mwanadada mmoja, kimwana na mrembo wa haja, aliyekuwa anatembea kwa mwendo wa kunata. Moja kwa moja akaenda kukaa kwenye meza iliyokuwa pembeni, jirani yake tu. Mara baada ya kukaa, kimwana huyo aliangaza macho pande zote kuangalia alipo mhudumu, na mhudumu alipomwendea, alimwangiza chakula, wali kwa nyama ya kuku, pamoja na soda moja aina ya Mirinda.



    Kimwana huyo alipohudumiwa chakula kile alichokuwa ameagiza, alinyanyuka na kunawa mikono yake katika sinki maalum lilokuwa umbali mfupi kutoka ilipokuwa meza yake. Alipomaliza kunawa, akarudi tena na kendelea kula taratibu, tena kwa mapozi ya hali ya juu, kwani hakuwa na haraka. Wakati wote huo alikuwa akiangalia chakula chake na wala hakuwa na muda wa kuangalia pembeni.



    John Bosho aliendelea kumwangalia kimwana huyo kwa muda wote, ikiwa siyo mara yake ya kwanza kumwona akiingia hotelini pale. Ni mara nyingi walikuwa wanakutana, yaani ni kama bahati vile, kwani kila mmojawapo anapoingia, basi hujikuta wote wameingia, tena kwa wakati mmoja kana kwamba walikuwa wameahidiana.



    Kwa kiasi fulani, mwanadada huyo mrembo wa nguvu, alikuwa amemwingia akilini John Bosho, kiasi cha kumfanya atamani kummiliki na awe wake. Hivyo akawa anageuza shingo yake mara kwa mara kumwangalia, na halikadhalika kimwana huyo alikuwa akimwangalia yeye, bila shaka akishangaa kwa kukutana kwao. Yeye John Bosho aliendelea kumkazia macho huku  akijaribu kumuundia tabasamu la nguvu, ambalo hata yeye aliliona na kulipokea kwa hisia kali.



    Hata hivyo, mara baada ya kulipokea tabasamu hilo, kimwana huyo aliendelea kula chakula hicho, alichokuwa anakula kama vile hataki. Hakika Mwenyezi Mungu alikuwa amemjaalia kimwana huyo sura nzuri ya mviringo, iliyobandikwa macho mazuri, makubwa kiasi, malegevu, ambayo kama ukiyaangalia tu, hujikuta mtu akitoa salamu kwake, hususan mwanaume.



    Kifua cha kimwana huyo mantashau, kilikuwa chembamba kilichobeba matiti madogo yaliyosimama wima, miguu yake ilikuwa minene kiasi iliyojaa nyama, na yenye matege ya kupendeza. Na miguu hiyo ikabeba makalio yaliyotuna kwa nyuma na kutikisika kila alipokuwa anatembea bila yeye mwenyewe kujua. Ni mtikisiko uliowaacha wanaume wengi wakiwa hoi kwa kudondosha udenda kwa kumtamani kimapenzi!



    Akiwa ni kijana mtanashati, mwenye nguvu za kiuchumi, John Bosho aliamua jambo moja tu. Ni kwenda kumwingia kimwana huyo, ili aweze kumwaga sera zake. Yeye akiwa ni mwanaume wa shoka, asiyeogopa watoto wa kike wa aina ile, akaamua kunyanyuka kutoka katika meza yake. Baada ya kunyanyuka, akaelekea katika meza ile aliyokaa mwanadada huyo, kama vile walikuwa wanafahamiana kwa muda mrefu.



    “Hali yako dada…” John Bosho alimsalimia huku akivuta kiti kimoja kilichokuwa upande wa mbele na kukaa huku wakitazamana.



    “Nzuri tu,” kimwana huyo alisema huku akimwangalia John Bosho alivyokuwa amekaa kwenye kile kiti kilichokuwa kinatazamana na yeye.



    “Samahani dada’ngu, nakaa kidogo bila idhini…” John Bosho akaendelea kumwambia huku akimtolea tabasamu jepesi.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kuwa huru, wala usijali…” kimwana huyo akamwambia kwa sauti nyororo ya kumtoa nyoka pangoni!



    John Bosho akakaa na kubaki akimwangalia!



    “Mimi nimekuja hapa kwa lengo moja tu,” John Bosho akamwambia na kuendelea. “Ni kufahamiana na wewe. Tukiwa sote kama  Watanzania tunaoishi katika nchi ya amani, ni muhimu kufahamiana…”



    “Unasema kufahamiana?” Kimwana huyo akamuuliza huku akiendelea kumwangalia kwa mshangao!



    “Ndiyo. Ni kufahamiana tu, na si vinginevyo…” John Bosho akajibu kwa sauti ya upole huku akiirekebisha tai yake.



    “Kwa hivyo umeona ufahamiane na mimi tu? Mbona humu hotelini wanaingia watu wengi tu?” Kimwana huyo akaendelea kumuuliza.



    “Nina maana yangu…” John akamwambia.



    “Maana ipi?”                          



    “Ni historia ndefu…”



    “Historia ndefu kivipi?”



    “Unajua ni mara nyingi huwa naingia humu hotelini kula chakula mida kama hii,” John Bosho akamwambia na kuendelea. “Lakini kila ninapoingia ni lazima nikuone na wewe unaingia. Nafikiri hata wewe umetambua hilo.”



    “Eeh,” kimwana huyo akacheka kidogo na kusema. “Kwa hivyo ni hilo tu?”



    “Ndiyo hilo tu. Naona kama nyota zetu zimelingana.”



    “Sijui kama zimelingana. Lakini poa, kufahamiana siyo vibaya…” kimwana huyo akasema huku akiendelea kukata nyama ya kuku kwa kisu, kwa mtindo ule wa kujifanya kama alikuwa ameshiba. Na hiyo ilikuwa ni kwa akina dada wengi wanaojiona wazuri!



    “Kwa jina naitwa John Bosho. Mimi ni Mtanzania, pia ni mfanyabiashara maarufu hapa Jijini Dar es Salaam, ninayeishi eneo la Ukonga. Bado sijaoa, niko ‘singo.’ Kadi yangu ya kibiashara hii hapa…” John Bosho akamwambia huku akifungua pochi yake iliyokuwa imetuna. Akatoa kadi moja ya kibiashara na kumpa. Ni kadi iliyokuwa na jina la kampuni, anuani, na namba za simu.



    “Ahsante sana,” kimwana huyo akasema. Halafu akaipokea ile kadi ya kibiashara na kuitia ndani ya pochi yake iliyokuwa pale juu ya meza upande wa kushoto. Kisha akamwangalia John Bosho kwa nukta kadhaa katika kumsoma. Ni kweli alikuwa ni kijana mtanashati!



            ********



    JOHN Bosho alikuwa ni kijana mwenye umri wa miaka ipatayo thelathini na sita mpaka arobaini hivi, akiwa ni kijana mwenye elimu ya kidato cha sita, aliyoipata katika Shule ya Sekondari ya Mirambo, Mkoani Tabora. Hata hivyo baada ya kuhitimu na kufaulu vizuri, alitakiwa kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuendelea na masomo zaidi.



    Lakini kwa sababu alizozijua mwenyewe, John Bosho hakuendelea na masomo, kwa kile alichokiona kama alikuwa anapoteza muda wa kuanza kuchakarika na maisha. Baadaye alijiunga na vijana wenzake na kujiingiza katika biashara za madini ya aina mbalimbali, dawa za kulevya, na nyinginezo haramu, zisizokubalika na jamii.



    Akiwa ni mtu aliyejipanga kisawasawa katika kufanya shughuli zake za haramu bila kujulikana, aliamua kushirikiana na vijana wake maalum anaofanya nao kazi, ambao pia walikuwa wakifuata amri yake bila kupinga.



    Vijana hao machachari na wasiokuwa na woga wa aina yoyote,  John Bosho aliwapata katika kona mbalimbali za jiji la Dar es Salaam baada ya kuhangaika sana, kwani kupata watu wa kukubaliana na amri utakayowapa  ni kazi sana. Na katika kujiimarisha katika shughuli zake za haramu, John Bosho aliamua kuwapa mafunzo maalum vijana wake, na kuweza kutumia silaha za moto, kama bunduki na bastola.



    Baada ya kuhitimu vizuri katika matumizi ya silaha,  John Bosho aliamua kuwatuma sehemu mbalimbali nchini na kufanya vitendo vya uhalifu, ikiwa ni uporaji kwa wafanyabiashara wakubwa wenye fedha, hasa wanaojihusisha na biashara za madini, huko Mererani, mkaon Manyara, utekeji nyara na nyingine. Baada ya kufanikiwa katika ukamilishaji wa kazi hiyo haramu, vijana hao humkabidhi mali yote yeye, anayepanga utaratibu wa mgawo.



    Kazi hiyo John Bosho alifanikiwa kuifanya kwa muda mrefu bila kushtukiwa, akionekana kama mfanyabiashara anayejihusisha na biashara maduka ya vifaa vya ujenzi. Alifanikiwa kufungua duka kubwa la vifaa vya ujenzi, katika mtaa wa Swahili, eneo la Kariakoo.



    Ni duka ambalo lilikuwa linauza vifaa vya ujenzi kwa ujumla likiwa limejaa bidhaa za aina mbalimbali zinzohusika na shughuli za ujenzi kwa ujumla, kama vile, saruji, mabati ya aina mbalimbali, nondo na vinginevyo. Yote ile ilikuwa ni kivuli tu, ili aweze kufanya kazi zake kwa ufanisi zaidi. Duka hilo lilijulikana kwa jina la  J. B. Enteprises Ltd.



    Mbali na duka kumiliki duka lile, pia, John Bosho alikuwa anamiliki bohari kubwa la kuhifadhia bidhaa zake, lililoko eneo la Ubungo Machimbo ya Mawe. Ni bohari ambalo alikuwa amelikodi kutoka kwenye kampuni moja ya ujenzi, kwa ajili ya kuhifadhi mizigo yake anayoiagiza kutoka nchi za nje. Ndani ya bohari hilo, palikuwa na ofisi ya kuratibu mipango yake haramu, anapokutana na vijana wake.



    Hakuna mtu yeyote ambaye angeweza kuwashtukia, John Bosho na wenzake, kwani walifahamika kama wafanyakazi wake waliokuwa katika mishughuliko ya kikazi. Alijitahidi sana kuratibu mipango yake bila kufahamika na kwa kiasi fulani alifanikiwa sana na kuendelea kujilimbikizia fedha na kufanya anachotaka, hata kujipatia wasichana warembo anaowataka!



          ********http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    JEURI yake ya fedha na kupenda wanawake, John Bosho alifanikiwa kumnasa mwanadada mmoja mrembo, aliyejulikana kwa jina la Helen Fataki, siku za nyuma. Huyo alikuwa ni mwanamke wa shoka na mfanyabisahara maarufu aliyekuwa katika umri  wa ujana, miaka ishirini na minane hivi.



    Baada ya kumnasa na kuendelea naye kimapenzi kwa muda, walikuja kushindana baada ya Helen kugundua kuwa yeye alikuwa ni mtu anayejihusisha na kazi za uhalifu. Hivyo basi, John Bosho akaamua kujiweka kando na kuendelea na shughuli zake za kibiashara ndani ya jiji la Dar es Salaam na hata nje ya nchi.



    Ingawa walikuwa wametengana, John na Helen walikuwa wanaishi kama ‘Paka’ na ‘Panya’, kwa kila mmoja akimwogopa mwenzake. John alimwogopa Helen asije akamchoma na kutoa siri zake kwa Jeshi la Polisi, juu ya kazi yake ya uhalifu aliyokuwa anaifanya, Helen Fataki naye alimwogopa John Bosho asije akamlipua na kumwondoa uhai ili asiweze kutoa siri zake nje, ambazo akiwa kama mpenzi wake, alikuwa anazifahamu!



    Ni mara nyingi John Bosho alikuwa akimtishia maisha kwa kumwonya kutoitoa siri ile kamwe! Hivyo Helen Fataki akawa ameshikwa pabaya, akautia mdomo wake kufuli kwa kutoitoa siri ile kwa mtu yeyote. Basi ukawa mchezo wa kuwindana, hadi John Bosho alipokutana na mwanadada yule, Anita, ndani ya Hoteli ya The Kibo II Anex muda na wakawa wanafahamiana kwa undani zaidi!



    Baada ya John Bosho kumkabidhi kadi yake ya kibiashara, mwanadada huyo akatabasamu kidogo, halafu akasema:



    “Nashukuru sana kwa kunipatia kadi yako ya kibiashara….”



    “Na mimi nashukuru pia, kwa kuipokea…” John Bosho akamwambia huku akiunda tabasamu pana.



    “Kwa jina naitwa Anita Anthony. Ninafanya kazi katika shirika moja lisilo la kiserikali. Bado sijaolewa…”  akajitambulisha mwanadada huyo, aliyejulikana kwa jina la Anita.



    Pia yeye akampatia kadi yake ya kibiashara kutoka katika pochi yake ndogo, aliyoitoa ndani ya mkoba wake uliokuwa pale juu ya meza.



    “Nashukuru sana kwa kunipatia kadi yako. Utanisamehe sana, lakini huu ndiyo mwanzo wa kufahamiana…” John Bosho akamwambia Anita.



    “Na mimi nashukuru pia…” Anita naye akamwambia huku akimwangalia kwa chati. Halafu akaendelea kumalizia chakula chake taratibu.



    Mwadada huyo mrembo, Anita Anthony, alikuwa amezaliwa na kukulia kwenye familia iliyojimudu kimaisha. Alikuwa ni mtoto wa pekee wa kike kwa wazazi wake, jambo ambalo lilimfanya alelewe kwa kudekezwa kidogo. Alizaliwa na kukulia eneo la Kiwalani, Jijini Dar es Salaam, akiwa na wazazi wake, Mzee Anthony Mkonyi na mama yake mzazi, Bi. Matilda Msechu, wakiwa na asili ya Mkoa wa Kilimanjaro.



    Pia, Anita alikuwa na kaka zake wawili waliomtangulia, waliojulikana kwa majina ya Peter na Joseph. Alipata Elimu yake ya Msingi, katika  Shule ya Msingi Uhuru Mchanganyiko, jijini Dar, ambapo baada ya kumaliza, alifaulu na kujiunga na Shule ya Sekondari ya Tambaza. Alisoma pale hadi alipohitimu kidato cha sita, ndoto ambayo alikuwa nayo muda mrefu hasa ukizingatia aliithamini elimu.



    Baadaye alijiunga na Chuo cha Uhasibu Chang’ombe na kufanikiwa kupata Shahada yake ya Uhasibu. Hakika Anita alifurahi sana na hatimaye akaajiriwa na Shirika moja lisilo la Kiserikali, akiwa katika kitengo cha fedha, kama  mtunza fedha. Ofisi ya shirika hilo, iko ndani ya Jengo la Shirikisho la Vyama vya Ushirika, lililoko mtaa wa Lumumba, eneo la Mnazi Mmoja.



    Anita aliipenda kazi hiyo na kuifanya kwa moyo mkunjufu, akiwa bado msichana mwenye umri wa miaka 26 hivi, mbichi kabisa. Tuseme alikuwa ni mtu mwenye kiu ya maendeleo, aliyependa kujiondoa katika tatizo la kuwa tegemezi. Hivyo basi, baada ya kukutana na John Bosho siku hiyo, naye alijikuta akimpenda kijana huyo mtanashati, ukizingatia naye alikuwa akimwona kila mara na kuridhishwa na ule utanashati wake.



    Baada ya John Bosho na Anita kufahamiana, walikaa pale hotelini kwa muda huku wakishushia chakula kwa vinywaji baridi, wakiongea hili na lile kama vile watu waliokuwa wamefahamiana muda mrefu. Walipomaliza wakaagana na kuahidiana kukutana siku nyingine, na hata kuwasiliana kwa mawasiliano ya simu zao za kiganjani.



    Anita alipotoka pale hotelini, alielekea ofisini, anakofanyia kazi, ndani ya Jengo la Shirikisho la Vyama vya Ushirika. Kwa vile hapakuwa mbali, alitembea kwa miguu tu huku wakiongozana na John Bosho. Walipofika nje, John Bosho akaliendea gari lake lililokuwa eneo la maegesho, akapanda na kuondoka kuelekea katika mishughuliko yake mingine ya siku ile.



     Anita alipoingia ofisini kwake, alikaa kitini na kufungua pochi yake aliyoitoa ndani ya mkoba. Akaitoa ile kadi ya kibiashara aliyopewa muda ule walipokutana na John Bosho, halafu akaiangalia kwa makini, na aliporidhika, akairudisha ndani ya pochi na kuendelea na kazi zilizokuwa zinamkabili.



    Ukweli ni kwamba, ingawa Anita alikuwa ameshampenda John Bosho Lakini hakuwa akimjua undani wake sana, kwa vile ilikuwa ndiyo mara ya kwanza wamekutana.



    *******     



    WIKI moja ilipita tokea John Bosho walipokutana na mwanadada, Anita Anthony, katika Hoteli ya The Kibo II Anex, walipokwenda kula chakula cha mchana. Tuseme walikuwa hawajaonana tena baada ya John kupata safari ya kikazi, katika kuratibu mipango yake, ukizingatia alikuwa ni mtu wa kusafiri sana.



    Lakini pamoja na kutoonana kwa muda wa wiki ile, kila mmoja alikuwa akimuwazia mwenzake. Ina maana John Bosho na Anita walikuwa wameshajenga kitu fulani ndani ya mioyo yao, yaani upendo wa dhati!



    Hivyo basi, siku ya Ijumaa majira ya saa sita na nusu za mchana,  Anita Anthony alikuwa ndani ya ofisi yake, akijiandaa kutoka, kwenda kupata chakula cha mchana. Mara simu yake ya mkononi aliyokuwa ameiweka juu ya meza iliita, na alipoiangalia namba za mpigaji, akaona ni John Bosho!



    Moyo ukamlipuka!



    “Haloo…Anita naongea…” Anita Anthony akasema kwa sauti ndogo lakini. Yenye kusikika kwa mtu wa upande wa pili.



    “Haloo…John Bosho hapa. Natumaini hujambo…” upande wa pili wa simu, John Bosho akasema.



    “Mimi sijambo…”



    “Nimeona nikupigie simu. Sijui leo una ratiba ya kwenda kula chakula cha mchana wapi?”



    “Nitakula palepale The Kibo II Anex Hotel…”



    “Leo usiende pale…”  John akamwambia.



    “Kwa nini nisiende pale?”



     “Mimi nitakupitia hapo ofisini saa saba mchana. Tutakwenda kula sehemu nyingine.”



    “Sawa, nitakusubiri.”



    “Ok, niko njiani…”



    Anita alisubiri akiwa palepale ofisini. Baada ya dakika kumi hivi, John Bosho akampigia simu na kumwambia kuwa alikuwa anamsubiri kwenye gari lililokuwa kule nje, kando ya Barabara ya Lumumba. Anita Anthony akauchukua mkoba wake na kushuka chini kwa kutumia lifti. Alipofika chini  akamkuta amelipaki gari kwenye maegesho akimsubiri, naye akaufungua mlango wa kushoto na kuingia ndani.



    Ile kuingia ndani ya gari tu, harufu ya mafuta ya uzuri  ikaenea ndani ya gari na kuishia  katika pua ya John, kiasi cha kumpa burudani ya pekee na pia hisia za mapenzi zikimwingia!



    “Habari za siku John…” Anita akamwambia punde tu baada ya kukaa.



    “Nzuri tu. Nimerudi katika safari yangu…”



    “Pole na safari…”



    “Nimepoa,” John Bosho akasema na kuendelea. “Nimeona nikupitie tukale ‘lunch.’ Sijui unapendelea hoteli gani yenye hadhi?”



    “Hoteli yoyote unayopenda wewe…” Anita akamwambia.



    “Ok, twende New Africa Hotel…au unasemaje?”



    “Hakuna shaka…tunaweza kwenda, ni katika kubadili uelekea…”



    John Bosho akaliondoa gari na kuelekea katikati ya jiji la Dar es Salaam. Ingawa foleni ya magari iliwasumbua, lakini walifika katika Hoteli ya New Africa, iliyoko katika makutano ya mitaa ya Azikiwe na Sokoine Driver. Ni sehemu iliyokuwa na msongamano mkubwa wa watu, wengi wao wakiwa katika mihangaiko yao ya kutafuta riziki.



    Baada ya kufika, John akalipaki gari katika sehemu ya maegesho iliyoko upande wa pili wa hoteli hiyo, halafu wakashuka na kuingia ndani.  Walifikia katika ukumbi wa chakula, uliokuwa katika hali ya utulivu kwa muda huo, ambapo walikaa na kuagiza  chakula walichopendea. Baada ya kuhudumiwa chakula, wakaendelea kula huku kila mmoja akiwa na mawazo yake kichwani.



    “Anita,” John Bosho akamwita kwa sauti ndogo.



    “Bee…” Anita Anthony akaitikia kwa sauti ndogo.



    “Nimekuomba tuje kula hapa tuje kula chakula cha mchana, na pia ili tuweze kuongea mawili matatu. Nafikiri unajua tokea tufahamiane hatujaongea mambo mengi…” John Bosho akamwambia.



    “Hiyo ni kweli kabisa, hatujaongea zaidi ya kusalimiana tu…”



    “Vizuri sana,” John Bosho akasema na kuendelea. “Hivi mwenzangu, hapa Dar es Salaam, unaishi sehemu gani?”



    “Mimi ninaishi eneo la Kiwalani…” Anita akasema.



    “Umepanga au umejenga nyumba?”



    “Hapana, bado sijafanikiwa kujenga,” Anita akasema huku akitabasamu. Kisha akaendelea. “Mimi naishi kwa wazazi wangu. Hivyo bado sijaanza maisha ya kupanga.”



    “Aisee, unaishi kwa wazazi?”



    “Ndiyo, kwani vipi?”



    “Hupaswi kukaa na wazazi wako,” John Bosho akamwambia na kuendelea. “Wewe ni mtu mzima unayepaswa kujitegemea na kujipangia mambo yako!”



    “Hilo naelewa sana…” Anita akamjibu huku akitoa tabasamu dogo.



     “Ndiyo hivyo, utakosa vingi!” John Bosho akaendelea kumwambia Anita, huku akionyesha ujivumi wa fedha!



    “Ni kweli unalosema. Lakini inabidi iwe hivyo, kwani niko peke yangu na sijaolewa, sasa haraka ya nini?” Anita akamwambia.



    “Lakini ukiolewa utahama hapo nyumbani kwa wazazi wako?”



    “Ndiyo, nitahama kumfuata mume.”



    “Je, ukichumbiwa na kupangiwa chumba, utakubali?”



    “Inategemea…” Anita akasema na kuongeza. “Mchumba akiwa mwaminifu nitakubali, maana siku hizi wanaume wengi siyo waaminifu kabisa…”



    “Una maana gani kusema hivyo?”



    “Nina maana kuwa, ninaweza kuchumbiwa na mchumba ambaye tutakuwa tumekubaliana. Halafu ananipangia chumba, kumbe mchumba mwenyewe anaweza kuja kuwa mwongo tu wa kunipotezea muda wangu, na baadaye kunitelekeza baada ya kunitumia vya kutosha!”Anita akamwambia John.



    “Unalosema ni kweli,” John Bosho akasema na kuongeza. “Lakini siyo wanaume wote wanaofanya hivyo.”



    “Na mimi sikusema wote, John…” Anita akamwambia baada ya kujua John alikuwa ana maana gani!



    Alikuwa anajipigia debe yeye mwenyewe!



    “Ok, tuyaache hayo. Je, unaweza kuwa na nafasi siku gani, ili tuweze kuongea mambo mengi na kufahamiana zaidi?” John Bosho akamuuliza Anita.



    “Siku ambayo nina nafasi, ni Jumapili…” Anita akamwambia.



    “Basi, nakuomba sana tukutane Jumapili inayokuja…”



    “Tukutane wapi?”



    “Naomba tukutane Zungwa Beach Hotel, Oysterbay. Hii ni sehemu iliyotulia sana, hakuna vurugu kama hoteli nyingine za uswahilini.”



    “Sawa, kama umechagua twende huko, mimi sina kipingamizi.”



    “Na kuhusu usafiri, nitakupitia sehemu, mbali kidogo na nyumbani kwenu, halafu tuongozane wote.”



    “Hakuna shaka, na mengine tutawasiliana kwa simu…”



    John Bosho na Anita walikaa hapo New Africa Hotel, huku wakiendelea kula na kunywa vinywaji baridi. Hapo waliongea mengi, hadi walipomaliza kula, ndipo walipotoka tayari kurudi katika sehemu zao za kazi, hivyo wakatoka nje tayari kwa kuondoka.



    Hakika John Bosho alikuwa ameridhika sana baada ya kukutana na kimwana yule aliyekuwa amemwingia rohoni mwake. Na zaidi ni ile kumkubalia kukutana naye siku ya Jumapili kule Zungwa Beach Hotel, ili aweze kumjulisha azma yake. Baada ya kupanda gari, wakaondoka kumrudisha Anita kazini kwake, na yeye akaendelea na shughuli zake. Alishaamua kufanya urafiki na Anita, na hata ikiwezekana awe mke wake hapo baadaye.



            *******



    SIKU ya Jumapili ilifika, na kama walivyokuwa wameahidiana, John Bosho na Anita walikwenda Zungwa Beach Hotel, iliyoko ufukweni mwa Bahari ya Hindi, kutembea na kupumzika katika kuifurahia mwisho wa wiki. Kama kawaida, John Bosho alimpitia nyumbani kwao, Kiwalani na kumchukua kwa gari lake.



    Siku hiyo Anita alikuwa ameupara vizuri na kuonekana ule uzuri wake waziwazi kitu ambacho kilimvutia sana John.Baada ya kufika kwenye hoteli hiyo ya kifahari, iliyoko ufukweni mwa Bahari ya Hindi, siyo mbali sana na ufukwe wa Coco, John alilipaki gari katika sehemu ya maegesho ambapo palikuwa na magari mengine.



    Baada ya kulipaki, wote wakashuka na kuelekea sehemu ya nyuma ya hoteli kwa mwendo wa taratibu kama vile wapenzi wawili wanaopendana, ambapo palikuwa na sehemu nzuri ya kupumzikia, iliyokuwa na mandhari nzuri hasa ukizingatia ilikuwa karibu kabisa na bahari.



    Sehemu hiyo waliyokuwa wamekaa John Bosho na Anita, palikuwa na viti vilivyokuwa ndani ya kibanda cha makuti, waliagiza chakula na vinywaji, ambapo waliendelea kula na kunywa taratibu. Hapo ndipo John Bosho alipoanza kumwaga sera zake kwa Anita, katika kumwingiza katika mstari ulionyooka.



    Vilevile walikuwa wakiongea mambo mengi na kujikuta wakiingia katika dimbwi la mapenzi, kwani kutokana na jinsi John Bosho alivyokuwa akipangilia maneno yake, na Anita alijikuta akikubali kila alichoambiwa. Walipomaliza kula na kunywa, walipanga chumba cha muda ndani ya hoteli hiyo ya kifahari, ambapo walipumzika humo na kujiliwaza kimapenzi kwa zaidi ya saa mbili.



    Walipomaliza starehe yao ya kiutu uzima, walioga na kuvalia tena nguo zao, halafu wakaondoka kurudi katikati ya jiji. Walisumbuliwa sana na foleni ya magari barabarani, lakini John alimrudisha Anita nyumbani kwao, Kiwalani, akiwa salama. Hakika, kwa upande wa John, alikuwa amefurahi sana baada ya kumnasa mwanadada huyo mrembo, ambaye alifanana na mazingira yake anayoishi, akiwa ni mtu mwenye fedha za kutakata.



    Kuanzaia hapo, John Bosho aliapa kuwa hatokubali ampoteze Anita, na atammiliki awe wake daima, na hakuna mwanaume mwingine atakayemwingilia katika penzi lake change!



            ********



    BAADA ya miezi mitatu hivi, John Bosho na Anita walishakuwa marafiki na kushirikiana katika mapenzi. Wakajikuta kila mmoja akimhitaji mwenzake, kwa kila anapopata nafasi.



    Hata hivyo ile kero ya kukutana katika mahoteli makubwa au katika n yumba za kupanga, kama vile Lojingi, hazikuwafurahisha wote wawili, hivyo John akaamua kumpangia Anita nyumba ya maana itakayomfaa, ambapo hakutaka apate shida.



    Anita alifanikiwa kupata nyumba ya kupanga eneo la Tabata Mawenzi, ambapo akiwa mpenzi wake, John Bosho, akiwa ni mtu anayefahamika sana, alitumia madalali maarufu, ambao walimtafutia nyumba hiyo iliyokuwa katika kiwango alichokipenda.



    Ni nyumba ndogo iliyojengwa kifamilia, ikiwa na vyumba viwili, sebule na stoo. Pia, huduma za choo zilikuwa mlemle ndani. Akalipa kodi ya mwaka mzima, na Anita akahamia mara moja, kutoka Kiwalani, nyumbani kwa wazazi wake alipokuwa anaishi kwa muda mrefu.



    Mbali ya kumpangia nyumba hiyo, pia alimnunulia samani zote za ndani. Ni samani alizozinunua katika duka moja linalouza samani za gharama, lililopo  katika Barabara ya Nyerere. Baada ya kumfanyia yote yale, sasa John akapumua na kufurahia kummiliki mwanadada yule mrembo aliyekuwa anamezewa mate na wanaume wengi!



    Kwa vile nyumba hiyo ilikuwa na usalama wa hali ya juu, John Bosho alikuwa anakwenda mara kwa mara na kupumzika, huku pia akijaribu kujikwepesha asijulikane na watu wengi sana ukiwa ndiyo utaratibu wake aliokuwa amejiwekea. Kufahamiana na watu ovyo, wataijua siri yake!



    Ni mtu wa aina gani!



            ********



    MARA baada ya John na Anita kuunganisha mahisiano na uchumba, Anita aliona ni vyema akutane na mama yake mzazi ili amfahamishe kuhusu jambo hilo ambalo kwa upande wake aliona kuwa ni la kheri kwani ni wanaume wachache sana siku hizi wanaopenda kuoa, na pia ni wanawake wengi ambao hawaolewi, hivyo ni bahati yake ya pekee ambayo kamwe hakupenda kuikosa.



    Hivyo basi, Anita alimwomba mama yake wakutane faragha ili aweze kumdodosea. Siku hiyo ya Jumapili walikutana ndani ya sebule nadhifu, nyumbani kwao Kiwalani, ambapo Anita alimtembelea mama yake huyo, Bi. Matilda, ukiwa ni utaratibu wake wa kawaida aliokuwa amejiwekea.



    Baada ya kufika pale nyumbani, aliwakuta wazazi wake, baba na mama yake ambao aliwasalimia, wakaongea mengi tu. Anita alihudumiwa kinywaji baridi huku akiendelea kunywa taratibu, na ndipo alipoanza kumweleza mama yake juu ya azma yake ile.



    “Mama, nimekuomba kukutana na wewe, kwani nina maongezi muhimu sana,” Anita alimwambia mama yake ambaye walikuwa wamekaa naye kwenye sofa kubwa hapo sebuleni.



    “Maongezi gani mwanangu,” mama yake, Bi. Matilda akamuuliza.



    “Napenda kukujulisha kuwa nimepata mchumba,” Anita akamwambia huku akiunda tabasamu pana.



    “Oh, umepata mchumba mwanagu?” Bi. Matilda, mama yake akamuuliza huku naye akiunda tabasamu pana.



    “Ndiyo, mama, si unajua umri unazidi kwenda?”



    “Ni kweli mwanangu, umri unazidi kwenda. Ni vizuri sana kama utaolewa mapema na kupata watoto mapema, kwani ukichelewa zaidi ya miaka mitatu kutokea sasa, basi ujue umezeeka! Itabidi uolewe na mtu wa makamo ambaye siyo kijana tena!”



    “Na ndiyo hilo sitaki mama…”



    “Basi, hilo ni jambo la heri,” mama yake akasema na kuongeza. “Lakini cha muhimu ni vyema kama unamuamini huyo mchumba, basi, afanye taratibu zote za kuja kujitambulisha kwetu na mambo mengine yafuata.”



    “Yeye pia ana hamu kubwa sana ua kuja kujitambulisha,” Anita akasema na kuongeza. “Ukweli ni kwamba ni mtu ninayemuamini, na siamini kama atakuwa ni mwanaume mwongo.”



    “Vizuri, nashukuru kwa kunieleza hayo. Mimi nitakaa na baba yako, halafu nimweleze jambo hili,” mama yake akamwambia kwa kumpa matumaini.



    “Sawa, mama, nitashukuru sana.” Anita akasema.



    Baada ya kumaliza mazungumzo yao ambayo hayakuichukua muda mrefu, Anita alibaki akimalizia kinywaji chake na pengine kuongelea mambo mengine yanayohusu maisha kwa ujumla.



    ********



    WALIONEKANA ni wapenzi wawili waliopendana sana. Kila sehemu, John na Anita walikuwa wakifuatana wote, iwe kwenye starehe au hata kufanya manunuzi katika maduka mbalimbali ya bidhaa za chakula na hata nguo na vipodozi, jijini Dar es Salaam.



    Baada ya mapenzi yao kukolea haswa, ndipo John Bosho alipofanya utaratibu mzima wa kujitambulisha kwa wazazi wa Anita. Alitafuta wazee wanaofahamika, akajitambulisha, utambulisho ambao ulifuatiwa na sherehe ndogo iliyofanyika katika ukumbi mmoja maarufu ulioko eneo la Kiwalani.



    Hivyo basi, kuanzia hapo John Bosho akawa anafahamika kama mchumba, na mume mtarajiwa wa Anita, mwanadada mrembo, aliyekuwa ana husudiwa na wanaume wengi, ambao nao walipenda wammiliki.  Na ili kuondoa udhia kabisa, akaamua kumvisha pete ya uchumba ya gharama kubwa, iliyotenezwa kwa dhahabu, ili ijulikane kuwa ni mchumba wake halali, asije akaporwa na wanaume wengine wenye uchu mkali.



    Mbali ya wazazi wake kumfahamu John, pia ndugu na jamaa nao walimjua kuwa alikuwa katika mpango wa kuja kumuoa Anita. Ikawa ni faraja kubwa kwa Anita kupata mchumba, heshima ikawa kwake, kwani aliheshimiwa na watu wote, wanaume kwa wanawake, kwa kujua sasa alikuwa amekata shauri la kuolewa na kuondokana na maisha yap eke yake.



    Hali ilendelea kuwa hivyo, na hata ofisini kwake alipokuwa anafanya kazi, wafanyakazi wenzake walikuwa wameshajua kuhusu mwenzao kupata mchumba, kiasi kwamba hata wale mabosi waliokuwa na kijicho pembe cha matamanio, waliacha kabisa tabia hiyo ya kumtaka kimapenzi!



    Mapenzi ya John Bosho na Anita yalikolea kadri siku zilivyokuwa zinakwenda. Muda wote huo, Anita alikuwa anajua kuwa mchumba wake huyo alikuwa ni mfanyabiashara mkubwa mwenye biashara nyingi, lakini upande wake wa pili hakuujua undani wake kwa vile alikuwa ni mtu anayefanya shughuli zake hizo kwa siri sana.



    ********     



    SIKU za nyuma, Anita na mwanadada, Getruda walikuwa ni marafiki wakubwa, waliokuwa wamesoma wote katika Shule ya Sekondari ya Tambaza, jijini Dar es Salaam. Lakini baada ya kumaliza masomo yao ya sekondari, kila mmoja aliendelea na shughuli zake, ambapo Anita alijiunga na Chuo cha Uhasibu, Chang’ombe, na Getruda akajiunga na kampuni moja ya simu za mkononi, akiwa Afisa Masoko.



    Hata hivyo urafiki wao ulikuwa haujafa, kwani walikuwa wakitembeleana mara kwa mara wanapopata nafasi. Walionekana kama vile walikuwa ni ndugu waliozaliwa tumbo moja, mambo yalikuwa hayohayo mpaka wakati mwingine walipojikuta wakiwa bize sana na shughuli zao, kiasi cha kutoweza tena kuonana mara kwa mara zaidi ya kuwasiliana kwa simu zao za mkononi.



    Siku moja ya Jumamosi, John Bosho, Anita na Getruda, walijikuta wamekutana katika viwanja vya starehe, wakijirusha na pengine kusuuza makoo yao kwa vinywaji. Walikutana kwenye Ukumbi wa Amana Club, Ilala, ambapo John Bosho alikuwa amekwenda na Anita kwa ajili ya kuburudika na Muziki wa Dansi wa Msondo Ngoma, unaoporomoshwa na Bendi ya Muziki wa Dansi ya Msondo.



    John Bosho alikuwa ni mpenzi wa ‘Msondo,’ ambapo hakupenda kukosa hata mara moja katika siku za mwisho wa wiki. Wakiwa wamekaa katika meza yao, Anita aliweza kumwona Getruda akicheza muziki akiwa peke yake. Akanyanyuka baada ya kumuaga John na kumwendea Getruda pale alipokuwa na kumshika begani.



    “Getu…” Anita akamwita kwa sauti ndogo huku akimgusa.



    “Oh, Anita…waooo!” Getruda akasema huku akinyanyuka na kumkumbatia Anita, na pia akishangaa kumuona katika eneo lile.



    “Za siku?”



    “Nzuri, sijui wewe?”



    “Mimi safi…”



    “Uko na nani?” Getruda akamuuliza Anita.



    “Niko na mchumba wangu, twende ukamfahamu…” Anita akamwambia huku akitabasamu!



    Wote wawili wakaongozana huku wameshikana mikono yao, hadi pale kwenye kiti alipokaa John Bosho. Wakasalimiana na kutambulishana.



    “Getu, huyu ni mchumba wangu, anaitwa John…” Anita akamtambulisha kwa mchumba wake.



    “Nashukuru sana kumfahamu…” Getruda akasema huku akimwangaliam John ambaye naye alikuwa anamwangalia kwa jicho la kisanii!



    “John, huyu ni rafiki yangu, anaitwa Getruda, ambaye tumesoma naye shule ya Sekondari…” Anita akamwambia John, ambaye bado alikuwa akimwangalia Getruda!



    “Nashukuru kumfahamu…” John Bosho akamwambia na kuendelea. “Anaishi wapi hapa jijini Dar es Salaam?”



    “Anaishi Ilala, mtaa wa Moshi…siyo mbali sana kutoka hapa Amana…” Anita akasema.



    “Oh, nashukuru sana,” John akasema huku akimpa mkono Getruda. Halafu akaendelea kusema. “Mimi ndiye John Bosho, kama ulivyotambulishwam, ninaishi huko Ukonga, lakini mwenzangu anaishi Tabata Mawenzi.”



    “Nashukuru kwa kufahamiana…” Getruda akasema huku bado akiwa ameunda tabasamu pana.



    Getruda alikuwa ni mwanamke aliyeumbika. Ni mwanamke mwenye lile umbile tata linalowasumbua wanaume wengi sana, akiwa amejaza makalio yaliyofuatiwa na nyonga iliyotanuka na umbile la namba nane! Kila akitembea makalio yalikuwa yanatikisika pasipo mwenyewe kupenda!

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hakika umbile hilo la Getruda, lilimsumbua sana John Bosho. Basi, tokea muda huo, akili yake ilikuwa haifanyi kazi tena baada ya kumwona Getruda akiwa na  lile gauni laini na la kubana alilovaa, ambalo liliruhusu mzigo wote wa makalio umwagike nyuma!



    Huo ulikuwa mtego!



    Siyo kwamba Anita alikuwa mwanamke mbaya ksura, kimaumbile au hata tabia, hasha. Isipokuwa ile ilikuwa ni tamaa ya wanaume wengi wasiokuwa na ustahimilivu baada ya kuona vitu kama vile! Lakini ukweli unabaki kwamba Getruda kwa usiku ule alikuwa tishio, na alimtamanisha kila mwanamke yeyote rijali!



    Usiku huo waliburudika kwa muda mrefu huku wakiongea hili na lile. Kwa wakati wote John Bosho alikuwa akicheza muziki na wanawake wote wawili, Anita na Getruda; wala Anita hakuwa na wivu wala kumtilia mashaka mchumba wake, kwamba anaweza kumtaka kimapenzi rafiki yake huyo, kumbe huku nyuma, John alikuwa ameshamhusudu Getruda, hivyo akaamua kuwa ni lazima ampate!



    Kazi hiyo!



    Ndipo John Bosho alipopata wasaa wa kumuulizia sehemu anayoishi, nyumba na mtaa. Bila kutambua nia yake, Getruda alimjulisha kuwa yeye anaishi mtaa wa Moshi, Ilala, nyumba namba 003. Mbali ya kumfahamisha sehemu hiyo anayoishi, pia walipeana namba za simu zao za mkononi, ambapo wangeweza kuwasiliana kwa kusalimiana na kutakiana heri kwa ujumla.



    Ukweli ni kwamba, Getruda hakujua kwamba John Bosho alikuwa ana nia mbaya dhidi yake, kwani alikuwa amechukua namba zake za simu ya mkononi, akiwa na lengo lake. Hivyo baada ya burudani ya muziki wa danisi kumalizika, ndipo wote walipoondoka kwa gari lao, ambapo John alimpitisha Getruda nyumbani kwake, mtaa wa Moshi, na kumwacha.



    Akiwa ni mwenyeji tosha ndani ya jiji la Dar es Salaam, John Bosho aliweza kuitambua ile nyumba aliyokuwa amepenga Getruda, akaitia alama kichwani mwake. Baada ya kumshusha Getruda, wenyewe wakarudi  Tabata Mawenzi, alikompangia nyumba Anita, tayari kwa kupumzika. Siku hiyo John Bosho alilala hukohuko nyumbani kwa Anita.



    ********     



    AKILI ya John Bosho hakutulia. Ilikuwa bado imezama kimapenzi kwa kimwana Getruda, rafiki yake mkubwa Anita, mchumba wake. Tamaa na uchu ulikuwa umemtawala pasipo kuweka tahadhari yoyote, hasa akilifikiria lile umbile tata alilokuwa nalo Getruda, ambalo likuwa limefichwa ndani ya magauni makubwa kama dera au nguo za kubana, kwa vyovyote alidhamiria kulionja.



    Akiwa ni mtu mwenye kujiamini, na mwenye fedha vilevile, John Bosho hakukaa kimya, kwani aliamua kumtafuta Getruda, rafiki yake Anita, ili amweleze azma yake ile ya kumtaka kimapenzi, hata kwa kutumia fedha. Wakati huo hakuona ubaya wowote kumtaka, kwani yeye aliamini kuwa ana haki ya kumtaka kila mwanake anapopenda! Hakuna kinachoshindikana mbele ya fedha!



    Kwa vile John Bosho alikuwa na namba za simu ya mkononi ya Getruda, basi akampigia na kumwomba wakutane sehemu watakayopanga, kwani alikuwa na mazungumzo naye, akiwa kama shemeji yake. Kwa vile Getruda hakumtilia mashaka, basi walikubaliana kukutana pale Msewa Bar & Lodging, iliyoko Buguruni, kunako majira ya saa moja za jioni. Hata hivyo, Getruda alikuwa akijiuliza kuwa John Bosho alikuwa anamwitia nini mpaka wakutane katika sehemu hiyo? Lakini akavuta subira mpaka watakapokutana.



    Getruda alipotoka kazini jioni, aliamua kupitia nyumbani kwake, mtaa wa Moshi, Ilala, kwanza, halafu akaoga na kuvalia nguo nyingine nadhifu ukizingatia sehemu yenyewe aliyokuwa anakwenda, ilikuwa na mkusanyiko wa watu wengi. Baada ya kumaliza kuvalia, Getruda akatoka na kutembea kwa miguu hadi alipofika katika barabara kuu ya Uhuru, inayotokea katikati ya jiji kuelekea maeneo ya Buguruni na kwingineko.



    Sehemu hiyo kulikuwa na teksi kadhaa zilizokuwa zimepaki zikisubiri wateja, hivyo Getruda akakodi teksi moja wapo na kumwambia dereva ampeleke Buguruni. Dereva akaiondoa teksi na kuifuata barabara ile ya Uhuru hadi alipofika Buguruni, eneo la Sokoni, halafu akamshusha Getruda. Sehemu hiyo palipokuwa na pilikapilika za watu wengi, hivyo nusu iliyobaki ambayo si mbali sana na ilipo Msewa Bar & Lodiging, alitembea kwa miguu kwa mwendo wa taratibu hadi alipoingia ndani ya baa ile maarufu.



    Alipoingia tu, akaangaza macho yake pande zote, lakini hakumwona John Bosho kama walivyoahidiana kukutana katika eneo lile la baa. Hata hivyo akachukua simu yake na kumpigia, ili kujua alipo kwa wakati ule, na John akamjulisha sehemu ile alipokuwa na kumwambia amfuate ndani ya chumba maalum kilichokuwa na huduma zote zinazohitajika.



     Ni chumba kilichokuwa upande wa nyuma ya baa ile, ambapo palikuwa na vyumba vingine kwa ajili ya starehe za muda mfupi au kulala mpaka asubuhi, hivyo Getruda akaelekezwa na wahudumu, na kupelekwa hadi kule nyuma ya baa, ambapo aliingia ndani ya chumba kile na kumkuta John Bosho amekaa kwenye sofa dogo, mbele yake kukiwa na meza ndogo iliyokuwa na vinywaji.



    Kilikuwa ni chumba kikubwa, kilichokuwa na seti moja ya makochi, friji ndogo, runinga, choo na bafu vilikuwa mlemle. Pia, palikuwa na sebule iliyokatwa kwa pazia kubwa lililotenga chumba kile, ambapo ndani kulikuwa na kitanda kikubwa cha futi sita kwa sita.



    “Karibu Getruda,” John Bosho akamwambia huku akitabasamu.



    “Ahsante…” Getruda akasema huku bado amesimama!



     Alikuwa akishangaa kumkuta shemeji yake huyo, John Bosho akiwa katika sehemu kama ile yap eke yake!



    Chumbani!



    “Mbona unasita?” John Bosho akamuuliza huku akinyanyuka kutoka pale kwenye sofa alipokaa.



    “Lazima nishangae…” Getruda akamwambia.



    “Unashangaa nini sasa?”                                           



    “Mbona hapa ni chumbani?”



    “Ndiyo, ni chumbani….” John Bosho akamwambia na kuendelea. “Ndivyo nilivyoamua, si unajua kuwa hapa kuna utulivu, tofauti na kule kwenye baa?”



    “Yaani umeniita kwa mazungumzo ya kuongelea chumbani?” Getruda akamuuliza.



    “Wala usihofu shem…” John akamwambia huku akimkalisha Getruda kwenye sofa lililokuwa pembeni.



    “Haya…nakaa..” Getruda akamwambia huku akikaa.



    “Hayo si ndiyo maneno?” John Bosho akamwambia huku naye akikaa kando yake. Chumbani hapo palikuwa kimya, isipokuwa ni sauti ndogo ya runinga ndiyo ilikuwa inasikika.



    Baada ya kukaa kwa muda, John Bosho aliagiza vinywaji na mapochopocho kwa mhudumu maalum aliyekuwa anamhudumia kila mara anapokuwa anafika hapo. Wakaendelea kula na kunywa na huku wakiongea mambo mengi tu, kitu ambacho kilimshangaza Getruda, kwani John hakumwambia alichokuwa anamwitia!



    “Shemeji John…” Getruda akamwita John kwa sauti ndogo.



    “Naam shem…” John Bosho akaitikia huku akimwangalia Getruda.



    “Naona muda unazidi kwenda…”



    “Ni kweli unakwenda…”



     “Basi, naomba unieleze ulichoniitia…”



    “Hakuna taabu. Nitakueleza tu…” John  Bosho akamwambia huku akiwaza la kufanya.



    Ni kweli kwamba John alikuwa amemwita pale kwa ajili ya mazungumzo maalum na yeye, lakini tokea amefika, ameshindwa kumwambia alichomwitia zaidi ya kuonyesha matamanio tu kuuangalia mwili wake! Kwa vile alikuwa amedhamiria kumpata kimapenzi, shemeji yake huyo, Getruda, aliamua kufanya kitu kimoja kibaya sana.



    Alipanga kuwa kabla ya kumwelezea kile alichomwitia, ni lazima afanye jambo fulani, ambalo litamlainisha mwanamke huyo aliyempania kupita kiasi. Yeye alikuwa ameshajiandaa kwa chochote tokea alipofika katika eneo lile husika. Hivyo aliamua kumtilia Getruda dawa ya usingizi, kwenye kinywaji chake, ambayo ni dawa yenye uwezo wa kumlegeza mwili wake haraka.



    “Hebu naomba unieleze shemeji, maana unaniweka roho juu kwa kusubiri…” Getruda akaendelea kumwambia John Bosho



    “hakuna taabu, shem, nitakueleza, kwani si jambo bay asana, mpaka likuweke roho juu sana…” John Bosho akamwambia.



    “Sawa, ngoja nikajisaidie, nikirudi basi unieleze ili roho yangu itulie…” Getruda akamwambia huku akinyanyuka kuelekea msalani.



    “Na kweli, utasuuzika na roho yako…”



    Hivyo basi, mara baada ya Getruda kwenda kujisaidia ndani ya choo kilichokuwa mlemle chumbani, John Bosho alibaki akishangilia sana, huku akirusha ngumi yake hewani, akijua kuwa sasa mpango wake utafanikiwa, ni lazima atafune kitu roho inapenda!



    Hakupoteza muda, kwani John alichukua ile dawa ya usingizi, iliyokuwa katika asili ya unga mweupe hivi. Akaunyunyuzia ndani ya glasi iliyokuwa na kinywaji alichokuwa anakunywa Getruda, halafu akamsubiri mpaka atakaporudi kutoka msalani!



          ********



    HAIKUCHUKUA muda mrefu, Getruda alirudi kutoka msalani. Akafikia tena kwenye sofa na kuiangalia glasi yake iliyokuwa na pombe nusu, lakini hakuinywa kwanza, bali alimwangalia John Bosho aliyekuwa anamwangalia kwa uchu mkubwa.



    Hata hivyo Getruda hakuweza kugundua mpango ule aliokuwa ameupanga John Bosho. Hivyo akainyanyua ile glasi na kunywa kinywaji kile cha bia kilichokuwa na mchanganyiko wa dawa ya usingizi aliyokuwa amemwekea, na alipomaliza kunywa, akaitua glasi chini.



    “Shemeji…” Getruda akamwita.



    “Naam…” John akaitikia.



    “Nafikiri mimi nikimaliza kinywaji hiki, naondoka…”



    “Unaondoka kabla sijakueleza nilichokuitia?”



    “Usiondoke,” John Bosho akamwambia na kuongeza. “Basi, nitakueleza, tega sikio!”



    Hata hivyo, kabla John hajaanza kumwelezea alichomuitia pale, dawa ile ikaanza kumlegeza na kumfanya kama amelewa kiasi cha kushindwa kustahimili, naye  John alipoona Getruda amelegea, ndipo alipoanza kumweleza alichomuitia.



    “Shemeji Getruda…” John akamwita.



    “Eeee…shem…” Getruda akaitikia kwa sauti ya kilevi.



    “Unajua nilichokuitia?”



    “Hapana…sijui…”



    “Nisikilize…”



    “Nakusikiliza…oh!”



    “Unajua nakupenda?”



    “Oh….unanipenda?”



    “Ndiyo. Nakupenda shem…”



    “Unanipenda kivipi?”



    “Nakuhitaji. Nataka uwe mpenzi wangu…”



    “Shemeji…ah! Haiwezekani…na Anita je?”



    “Mambo ya Anita achana naye kwa wakati huu!”



    “Nisijali vipi wakati ni mchumba wako?” Getruda akasema na kuongeza. “Isitoshe ni rafiki yangu!”



    “Nimeshakwambia hayo usijali…”



    “Ah, shem unaniweka katika wakati mgumu…”



    John Bosho akiwa na ulimi wa kushawishi, kubembeleza na pia ukichangia na ile dawa aliyomwekea Getruda ndani ya kinywaji chake, akaendelea kumbembeleza. Akahamia katika sofa alilokalia Getruda, akifanikiwa kumshawishi na kukubaliana kukutana kimapenzi! Dakika tano zilizofuata, wote walikuwa wameshasaula nguo zao na kubaki kama walivyozaliwa!



    Wakajikuta pia wakigaragara katika kile kitanda kikubwa cha futi sita kwa sita ikifuatiwa na miguno hafifu ya kimahaba mazito! Baada ya kumaliza ile mechi nzito, kila mmoja alijitupa kivyake na hatimaye Getruda kupitiwa na usingizi mzito kutokana na ile dawa aliyokuwa ametiliwa kwenye kinywaji.



    John Bosho aliufurahia ule ushindi wa kumpata kiumbe yule husika aliyekuwa na matamanio naye kwa muda mrefu, akajipongeza kwa hilo huku akiendelea kumwangalia zaidi na zaidi pale juu ya kitanda alipokuwa amejilaza Getruda katika umbile lile la utupu alilokuwa nalo! Ni hatari sana!



    Getruda alijikuta akilala ndani ya chumba kile alichopanga John Bosho. Ni mpaka ilipotimu saa nne za usiku ndipo aliposhtuka kutoka kwenye usingizi mzito na kujikuta amelala kwenye kitanda kimoja na John, shemeji yake! Ni usaliti wa hali ya juu!



    “Oh! Shem John!” Getruda akaita huku akinyanyuka kutoka pale kitandani nusu akipepesuka!



    “Naam,” John Bosho akaitikia huku akimwangalia kwa kijicho pembe!



    “Aisee? Umefanya nini?” Getruda akamuuliza huku akijiangalia katika hali ile ya utupu aliyokuwa nayo!



    “Kwani vipi?”



    “Huoni kama tumemsaliti Anita?”



    “Kumsaliti?”



    “Ndiyo manaake!”



    “Hayo usijali sana…” John Bosho akasema huku akitabasamu na kuonyesha ujivumi kwa kumpata na kujifurahisha kingono!



    “Nimefanya kosa kubwa sana…haya… nirudishe nyumbani!” Getruda akasema huku amechukia!



    “Nenda kaoge mpenzi…” John Bosho akamwambia.



    “Mpenzi tena…ala!” Getruda akamwambia huku akijifunga taulo kubwa.



    “Kwani kosa kukuita mpenzi?”



    “Ah, tuyaache hayo!”



    Getruda akaingia bafuni ambapo alioga haraka haraka na kutoka. Halafu John naye akaingia na kuoga, huku akimwacha Getruda akijiandaa kuvaa nguo zake. Baada ya kumaliza kuvalia, wakatoka hadi nje ambapo walipanda gari la John, tayari kwa kumrudisha Getruda nyumbani kwake, mtaa wa Moshi, Ilala.



    Walipofika nyumbani kwa Getruda, ilikuwa imetimu saa saa tano za usiku, na pilikapilika za watu zilikuwa bado zinaendelea katika mitaa ile ya Ilala, na nyumba aliyokuwa anaishi Getruda, ilikuwa bado haijafungwa.



    Kabla ya kushuka garini, John Bosho akamkabidhi Getruda kitita cha fedha,  shilingi laki tatu, ambazo zilitosha kumlegeza. Akasahau mambo yote yaliyotokea nyuma, na wala hakugundua kama John alikuwa amemtilia dawa ya kulevya katika kinywaji chake ili aweze kutimiza azma yake ya kufanya naye mapenzi!



    Basi, tokea siku ile ndiyo ukawa mchezo wao, ambao uliwafanya wanogewe na kuwa wanakutana mara kwa mara kwenye nyumba mbalimbali za wageni na kuivunja amri ya sita. Hata hivyo iliwabidi wafanye mambo yao kwa siri sana, ili Anita asiweze kuwashtukia, wakijitahidi kusafiri sehemu za mbali na kukamilisha kiu yao.



    Kutokana na ubize aliokuwa nao Anita, hakuweza kuwashtukia kabisa, kama rafiki yake mkubwa, Getruda, alikuwa amemchukulia mchumba wake, John Bosho. Kila mmoja aliendelea na shughuli zake na siku zikawa zinasonga mbele. Lakini hakuna marefu yasiyokuwa na mwisho!



            ********



    JUMATATU moja ambayo ni mwanzo wa wiki, Anita alikuwa amekaa ndani ya ofisi yao, pamoja na mfanyakazi mwenzake, Magret. Alionekana ni mtu mwenye mawazo mengi sana tangia alipoingia kazini asubuhi, kiasi cha kushindwa hata kufanya kazi. Pia, alikuwa ni mtu wa kujifyonza mwenyewe, ikionyesha kuwa kuna kitu alikuwa anawaza!



    Ndipo Magret alipoamua kumsogelea karibu ili amuulize kulikoni mpaka awe katika hali kama ile ambayo siyo kawaida yake. Anita siku zote alikuwa ni mtu mcheshi na mchangamfu kwa kipindi chote cha kazi, na kila mmoja alimzoea hivyo.



    “Vipi Anita, unaumwa?” Mage alimuuliza.



    “Hapana, mimi siumwi…” Anita alimwambia Magret huku akimwangalia kwa sura ya huzuni.



    “Sasa mbona uko katika hali kama hii?” Magret akaendelea kumuuliza.



    “Ah, wewe acha tu Mage…” Anita akasema kwa sauti ndogo ya huzuni.



    “Niache nini wakati nakuona hauko sawa?”



    “Ni kweli Mage…siko sawa…”



    “Ni kitu gani kinakusumbua?”



    “Kuna kitu kinanisumbua,” Anita akamwambia na kuongeza. “Lakini hakifai kuongelea hapa ofisini Magret.”



    “Kwa hivyo tukaongelee wapi?”



    “Naona twende hapo The Kibo II Hotel, ambayo ni sehemu nzuri…” Anita alimwambia huku akinyanyuka kutoka kwenye kiti.



    “Haya, twende…” Magret akamwambia Anita.



    Anita na Magret walitoka pale ofisini na kuelekea The Kibo II Anex Hotel, ambayo haikuwa mbali na pale. Baada ya kuingia ndani, wakaagiza vinywaji baridi na kuendelea kunywa taratibu.



    “Ndiyo ndugu yangu, naona kuwa huu ni muda muafaka wa kunielezea kilichokusibu…” Magret akamwambia Anita.



    “Ni sawa, inabidi nikuelezee kila kitu, kwa vile wewe ni mtu wangu wa karibu…” Anita akamwambia Mage huku uso wake ukionyesha bado kuwa na huzuni.



    “Nieleze mwaya, huwenda nikapata wazo la kukusaidia…”



    “Hivi si unajua kuwa nina mchumba?”



    “Ndiyo, najua kuwa unaye mchumba.”



    “Lakini tatizo ni kwamba mchumba wangu huyo ananipa taabu sana.”



    “Shida gani tena?”



    “Ananitesa sana, sijui kwa vile anajua kuwa ninampenda? Maana nasikia anajihusuisha kimapenzi na shoga yangu, Getruda…”



    “Unasema kweli?”

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ninasema kweli, kwa sababu siku hizi ninaona wana ukaribu mkubwa sana.”



    “Hali hiyo imeanza lini?”



    “Imeanza mara baada ya mimi kumtambulisha kwake.”



    “Je, una uhakika wana mahusiano?”



    “Dalili zinaonyesha na pia nimeshauona ujumbe wa simu kwenye simu ya John Bosho. Hata hivyo alijitahidi kuukwepesha.”



    “Ulishawahi kumuulizia Getruda juu ya tuhuma hizo?”



    “Hapana, sijamuuliza…”



    “Vizuri sana. Usimuulize kwanza, jaribu kufanya upelelezi kwanza na utakapogundua, ndipo utakapomweka kitako na kumuuliza.”



    “Sawa Mage, nitajitahidi kufanya upelelezi juu ya hayo. lakini roho inaniuma sana… si unajua kuchukuliwa mwanaume kunavyouma?”



    “Ni kweli kunauma sana, lakini ushauri ndiyo huo, fanya upelelezi kwanza! Mambo mengine yatafuata.”



    “Sawa, nitafanya hivyo.”



    Baada ya kumaliza mazungumzo yao, Anita na Magret walitoka pale hotelini na kurudi ofisini kwao. Kwa kiasi fulani Anita alikuwa ameridhika na tabasamu pana lilionekana usoni mwake.



    ********



    HAKUNA siri ya watu wawili duniani. Anita alikuja kuujua ule uhusiano wa kimapenzi baina ya Getruda na mchumba wake, John Bosho. Aligundua hilo baada ya kudokezewa na kijana mmoja, mwendesha bodaboda, aliyeujua uhusiano ule usiokuwa rasmi. Yeye alikuwa akimbeba mara kwa mara  Anita, kumpeleka katika sehemu mbalimbali ambazo alihitaji kufika haraka.



    Basi, akiwa katika kazi zake za kubeba abiria, ndipo kijana huyo alipoweza kuuona ule uhusiano wa Getruda na John Bosho, walivyokuwa wakijirusha na kutanua. Roho ikamuuma sana  kwa vile alikuwa anamheshimu Anita kama dada yake wa kuzaliwa tumbo moja. Hakuvumilia, hivyo akaamua kummwagia siri ile!



    Kijana huyo mwendesha bodaboda maarufu, alijulikana kwa jina moja tu, Don, ambalo ni jina alilokuwa amekatiwa na vijana wenzake wa mtaani, na wala jina la pili halikujulina. Yeye alikuwa akifanya kazi ile kati ya maeneo ya Buguruni Shell na maeneo ya Tabata, na mara nyingine sehemu mbalimbali za jiji, kama atakuwa amepata mteja wa kumpeleka huko.



    Baada ya Don kumfikishia ujumbe huo Anita, alimshukuru sana kwa kumtoa tongotongo machoni mwake, kwani alikuwa hajui kitu kama hicho. Hivyo akaamua kuufanyia kazi, na pia kupanga kumpa kazi nyingine ya kuendelea kumpeleleza John Bosho bila yeye kufahamu. Vilevile hakuacha kumjulisha rafiki yake, Magret juu ya kuinyaka siri hiyo, ambaye naye alimpatia ushauri wake, kuwa ni vyema angeanza kufanya upelelezi wake binafisi, na hata kumtumia Don.



    Na kweli, Anita aliamua kuanza kufanya upelelezi huo mara moja, baada ya kupewa ushauri na huyo Mage, mfanyakazi mwenzake. Pia, kwa bahati nzuri  Don, naye alikuwa anaujua uhusiano wa Anita na John, kama ni mtu na mchumba wake na mara nyingine aliwaona wakiambatana wote katika kilele cha mapenzi yao.



    Hivyo basi, siku moja Anita alimkalisha kitako Don na kuanza kuongea naye kumwelezea masahibu yaliyompata, ambapo alitaka msaada wake wa hali na mali katika kukamilisha upelelezi wake.



    “Kaka yangu, Don…” Anita alianza kumwambia.



    “Naam, dada yangu,” Don aliitikia huku akimwangalia kwa makini.



    “Samahani sana, leo nina mazungumzo muhimu sana na wewe,” Anita akaendelea kumwambia Don.



    “Mazungumzo gani dadangu?”



    “Ni mazungumzo yanayonihusu mimi na mchumba wangu, John Bosho. Natumaini unatambua kuwa uhusiano wangu naye.”



    “Ndiyo, uhusiano wako na John mimi naufahamu…”



    “Hivyo basi, nakuomba nikushirikishe huenda ukanipa ushauri cha kufanya…”



    “Unaweza kunieleza dada, kama kuna ushauri bila shaka nitakueleza cha kufanya.”



    “Natumaini unamfahamu vizuri mchumba wangu, John Bosho…”



    “Ndiyo, namfahamu. Si yule anayeendesha gari aina ya Toyota Harrier?”



    “Ndiye huyo huyo!” Anita akamwambia na kuendelea. “Ni mchumba wangu, ambaye tumevishana pete za uchumba. Lakini mwenzangu kwa kiasi fulani amekuwa siyo mwaminifu, nasikia anatembea na rafiki yangu, Getruda, anayeishi kule, Ilala!”



    “Unasema kweli dada?” Don akamuuliza huku ameachama mdomo!



    “Ni kweli kabisa. Hivyo basi, nakuomba uwe unafuatilia nyendo zao kwa vile wewe ni dereva wa pikipiki, hawataweza kukushtukia kamwe. Na hiyo ni ili tujue kama kinachozungumzwa ni kweli wana mahusiano, najua kwa vile unayo hiyo pikipiki, kazi haitakuwa ngumu sana. Hilo ndiyo ombi langu, siyo kama ninakulazimisha,” Anita akamaliza kusema huku akimwangalia kwa uchungu mwingi Don.



    “Nimekuelewa dada Anita, kwa hicho ulichonieleza. Kumbuka kuwa mimi ni mwanaume, na sipaswi kuwa mmbea, lakini kwa shida uliyoipata, sina budi kukusaidia…” Don alimwambia Anita.



    “Nitashukuru sana,” Anita akasema huku akitabasamu tabasamu la uchungu.



    “Tena,” Don akaendelea kusema. “Mimi nimeshawahi kuwaona wakiwa katika sehemu mbalimbali za stareha, lakini sikujua kama walikuwa na mahusiano ya kimapenzi kabisa. Lakini maadam aumeniambia hivyo, sina budi kukusaidia…” Don akaendelea kumwambia Anita.



    “Nitashukuru sana kakangu. Fuatilia na kila utakachokiona, nifahamishe, nitakutoa kwa chochote…” Anita akamwambia Don.



    “Ah, hayo usijali dada, wewe wangu,” Don akamwambia.



    Baada ya maongezi yao, Anita na Don waliagana kila mmoja akaendelea na shughuli zake.



    Siku hiyo ikapita!



    Mara baada ya Anita kuzipata taarifa za mchumba wake, John Bosho, alichanganyikiwa sana. Ili kuuokoa ule uhusiano wao wa uchumba, alimkabili na kumuulizia kuhusu tetesi zile, lakini John aliruka na kusema kwamba yale yalikuwa ni maneno ya watu tu yasiyowatakia maendeleo yao. Kamwe John  hakukubali kabisa kujihusisha kimapenzi kwa rafiki yake, Getruda.



    Anita alinyamaza kimya huku akiendelea kufanya uchunguzi wake. Daima alijua kuwa njia ya mwongo ni fupi, na iko siku lazima atakuja kuwafumania wakiwa wawili, ndiyo, ni lazima!



    Aliapa!



    ********



    MIEZI mitatu ilipita tokea John Bosho na Anita walipoanza kuulizana juu ya ule usaliti wa mapenzi uliokuwa ukifanyika. Hata hivyo kila mmoja aliendelea na kazi, ambapo Anita alikuwa alijaribu kwa hali na mali kuyasahau yale yaliyopita nyuma, hasa ukizingatia kazi aliyokuwa anafanya, ilikuwa ikimweka bize sana.



    Kila alipokuwa anatoka kazini huwa anachoka sana kiasi kwamba akifika nyumbani ni kupika, kuoga na kulala, basi. Lakini siku moja akiwa kazini, Anita aliupata ujumbe wa maandishi kwenye simu yake ya mkononi, kutoka kwa mwendesha bodaboda, Don, aliyekuwa anampa habari za mwenendo wa John Bosho na Getruda.



    Ni ujumbe ambao uliozidi kumtia jereha moyoni mwake, hasa ukizingatia alikuwa ameshaanza kusahau! Ujumbe ule ulisomeka kwenye kioo cha simu, “Tafadhali dadangu, Anita…nenda Max Bar, Ilala, utawakuta John na Getruda, usifanye fujo. Ninachotaka ni uhakikishe kuwa mchumbako anakusaliti…”



    Baada ya kuusoma ujumbe ule, Anita alichanganyikiwa sana, na hamu ya kufanya kazi ikamwisha. Akaamua kuaga kazini, akidai alikuwa amepigiwa simu ya dharura kutoka nyumbani. Akauchukua mkoba wake na kuupachika kwapani na kushuka kwa lifti hadi alipofika chini kabisa katika ghorofa ya mwisho. Akaelekea katika maegesho ya teksi yaliyoko upande wa pili wa Barabara ya Lumumba. Akakodi teksi hiyo impeleke Ilala, wakati huo ikiwa ni saa tisa za alasiri.



    Anita alikuwa ameamua jambo moja tu, kuwafuata na kuwavamia ili wajue kwamba alikuwa ameshawashtukia, na pia auvunje uhusiano wa uchumba mara moja, ikiwa ni pamoja na kuivua ile pete ya uchumba na kumrudishia John Bosho. Kutokana na usumbufu wa foleni ya magari barabarani, hatimaye wakafika Ilala, kando ya Barabara ya Uhuru, na pale Anita akashuka na kumlipa dereva nauli yake, na yeye akachanganya miguu kuelekea usawa wa mlango wa kuingilia ndani ya Max Baa.



    Mapigo ya moyo wake yaliongezeka na mwili kumtetemeka kwa hasira, lakini kila mtu aliyekutana naye, hakuna aliyemshtukia kama alikuwa katika hali kama ile. Alasiri hiyo wateja walikuwa ni wengi ndani ya baa ile maarufu, ambayo hutumiwa na wafanyabiashara wengi wanaoingia kuburudika baada ya shughuli za kikazi za kila siku.



    Baada ya kuingia ndani, Anita aliyatupa macho pande zote za mle ndani ya baa, na kwa bahati nzuri alimwona Getruda na John wamekaa kwenye kona iliyokuwa upande wa kushoto, karibu kabisa na kaunta ya kuuzia vinywaji. Hasira zikaongezeka, hivyo akaanza kuvuta hatua moja baada ya nyingine kuwafuatilia pale walipokuwa wamekaa!



    Ni kuanzisha tibwili!



          ********



    JOHN Bosho na Getruda walikuwa wamezama katika mazungumzo yao, huku Getruda akiwa amempa mgongo, na John Bosho amekaa upande wa nyuma akiangalia watu wanapoingia. Meza yao ilikuwa na chupa kadhaa za bia, ambao walikuwa wanakunywa.



    Kwa muda ule nishai ya pombe ilikuwa imeshaanza kuwaingia wote hasa ukizingatia walikuwa wameanza kunywa muda mrefu, tokea saa nane za mchana,  ikiwa ni yeye John aliyemwita Getruda baada ya kumpigia simu na kumsisitiza wakutane hapo! Ama kweli alikuwa ameshanogewa naye!



    John Bosho alikuwa wa kwanza kumwona Getruda alivyokuwa anaingia. Akashtuka na kujiuliza imekuwaje awe pale kwa muda ule? Hata hivyo  akabaki akimwangalia jinsi Anita alivyokuwa anawajongelea. Getruda naye alishangaa baada ya kumwona John amepigwa na bumbuwazi huku akiangalia nyuma yake! Ndipo naye akageuka kuangalia nyuma!



    Akamwona Anita!                                                                  



    Akashtuka sana!



     Abaki ameachama mdomo wake!



    Anita akavuta kiti  na kukaa huku akipumua kwa nguvu!



    “Habari zenu…” Anita akawaambia huku akiwa bado amesimama karibu yao.



    “Nzuri…karibu…” John Bosho akajitutumua na kumwambia. Lakini Getruda alinyamaza kimya huku akiiona ile hatari iliyokuwa inamkabili, kwa kusimamiwa na rafiki yake mkubwa, ambaye alionyesha dhahiri alikuwa ana hasira kali!



    “Naona wenzangu mnaburudika…”  Anita akaendelea kuwaambia.



    “Ah, ndiyo hivyo. Tunapooza makoo baada ya shughuli za kazi…” John Bosho  akasema huku akijiumauma!



    “Getruda,” Anita akasema huku akimgeukia.



    “Bee…” Getruda akaitikia huku aiangalia chini.



    “Naona umeamua kustarehe na shemeji yako…”



    “Ndiyo shoga’ngu…tumekutana tu…”



    “Si kweli…” Anita akasema na kuonyesha kutomwamini Getruda.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Huo ndiyo ukweli…nimekutana naye tu, ndiyo maana nikamkaribisha, na mimi sioni ubaya wowote!” John Bosho akadakia!



    “Ukweli sasa umejulikana!” Anita akasema na kuongeza. “Nilikuwa nakueleza John, kuwa una uhusiano na shoga’ngu, lakini ukanibishia. Sasa nimewakuta!”



    “Yaani kutukuta tumekaa wote ndiyo useme kuwa tuna uhusiano?” John Bosho akamuuliza Anita!



    “Ndiyo maana yake…” Anita akamjibu!



    “Kwa hivyo?” John akauliza.



    “Hakuna cha zaidi, mimi naona kuwa, wewe uendelee na rafiki yangu, Getruda, na mimi niendelee na ustaarabu wangu!” Anita akamwambia kwa hasira John!



    “Usifanye hivyo Anita. Mbona unataka kujaza inzi hapa?”



    “Ndicho ulichokitaka wewe…”



    Wakati wote huo, Getruda alikuwa amenyamaza kimya huku bado akiwa na wasiwasi. Ukweli ni kwamba alikuwa amechanganyikiwa sana, akitamani ardhi ipasuke ajichimbie! Lakini uzuri mmoja ni kwamba Anita akiwa mtu msomi, hakupenda kuzozana mpaka kila mteja aliyekuwa mle ndani ya baa ile ajue kuwa walikuwa wanagombana.



    Hivyo basi, Anita aliongea kwa upole huku pia roho ikimuuma sana, na baada ya kumaliza kuwapasha, akauchukua mkoba wake na kuondoka huku akiwaacha John na Getruda wakiwa wanashangaa!



    Ukweli ni kwamba lilikuwa fumanizi la nguvu!



    “Unaona sasa?” Getruda akamuuliza John!



    “Nimeona nini?” John Bosho akamuuliza!



    “Si mchumba’ko Anita katukuta? Sijui nani kamwambia tuko hapa?” Getruda akaendelea kusema huku akiwa na wasiwasi mwingi sana!



    “Si bure,” John Bosho akasema na kuongeza. “Inawezekana kuna mtu anafuatilia nyendo zetu!”



    “Basi, nimetosheka. Sina hamu na kinywaji, mimi naondoka kwenda nyumbani…” Getruda akamwambia John.



    “Sawa, tuondoke,” John akasema huku wote wakijiandaa kutoka.



    John Bosho na Getruda wakanyanyuka huku wakiacha baadhi ya vinywaji vyao juu ya meza, ambavyo vilikuwa havijamalizika. Kwa mwendo wa taratibu wakatoka hadi nje ya Max Bar, mita chache tu kutoka katika Barabara ya Uhuru iliyokuwa inakatiza mbele ya baa hiyo maarufu.Wakati huo ikiwa imetimu saa moja za usiku, hivyo wakaelekea sehemu ya maegesho alipokuwa amepaki gari lake, ambapo walipanda na kulitoka eneo lile.



    John Bosho alimpitisha Getruda nyumbani kwake, Ilala, mtaa wa Moshi, na kumwacha akiingia ndani, halafu yeye akaondoka huku nafsi yake ikimsuta kwa kitendo kile cha kukutwa akiwa na Getruda. Kwani ule ulikuwa siyo uaminifu angali akijua alikuwa na mchumba wake, Anita, waliokuwa wakitarajia kufanya utarataibu wa maandalizi ya kufunga ndoa.



    Ni usaliti!



    Hata hivyo, baada ya John Bosho kumfikisha Getruda nyumbani kwake, alipanga kwenda Tabata Mawenzi, nyumbani kwa Anita, usiku ule ule ili akamwombe radhi kwa kitendo kile alichokuwa amemfanyia. Ndiyo, alijiamini kuwa angemwagia maneno matamu ya kimapenzi ambayo yangemlainisha na kumfanya asahau masahibu yaliyomkuta!



    ********         



    ANITA alikodi teksi punde tu baada ya alipotoka ndani ya Max Bar. Hakupenda kukaa muda mrefu katika eneo hilo kwa jinsi alivyokuwa amechukia, na alijua kuwa inawezekana John akamfuata nyuma na kuanza kumbembeleza kama ilivyo kawaida yake, ndiyo maana akapenda aondoke eneo hilo haraka sana.



    Teksi iliondoka hapo Ilala, na kuifuata Barabara ya Uhuru, ambayo kwa muda huo ilikuwa na foleni kubwa ya magari. Anita alikuwa amekaa kwenye kiti cha nyuma huku amejiegemeza kama mtu anayelala. Hakika hakuamini kile alichokiona kwa macho yake, na hata teksi ilivyokuwa inaendelea na safari kuelekea Tabata, hakuwa na habari kabisa zaidi ya kuzama katika mawazo mazito.



    Teksi ilimfikisha nyumbani kwake, Tabata Mawenzi, bila yeye kufahamu kutokana na kuwa na mawazo mengi sana. Ni dereva aliyekuwa anaendesha ndiye aliyemshtua na kumuuliza kuwa anashukia wapi. Ndipo aliposhuka na kulipa fedha, kisha nusu iliyobaki akatembea kwa miguuu kwa kuufuata uchochoro unaolekea nyumbani kwake, ambao unapitia nyuma ya Mawenzi Bar.



    Baada ya kufika katika eneo la nyuma yao, akaingia ndani kwa kupitia katika mlango mdogo ulioko katika geti dogo lililotokeza uani. Kisha akaiendea nyumba yake iliyokuwa kule uani, ambayo ni kati ya nyumba zilizojengwa kwa kila mpangaji kujitegemea, inayofahamika kama ‘appatment,’ na kuzungushiwa uzio uliokuwa na urembo wa matundu yanayowezesha kuona upande wa nje.



    Nyumba yake aliyopanga, ilikuwa imejengwa kifamilia, ikiwa na vyumba vitatu, sebule, stoo, jiko na huduma ya choo ikiwa mlemle ndani. Mlango mkubwa wa kuingilia ulikuwa upande wa nje kutazamana na uwanja mdogo uliokuwa na bustani nzuri ya maua na miti iliyofungamana na kufanya kuwe na kivuli kizuri wakati wa mchana. Pia, eneo zima lilikuwa limezungukwa na huo ukuta madhubuti.



    Anita akatoa ufunguo ndani ya mkoba na kuufungua mlango ule mkubwa. Akaingia ndani na kupokewa na ukimya wa aina yake ukizingatia alikuwa anaishi peke yake. Baada ya kuingia ndani, akawasha taa, halafu akafikia kukaa kwenye sofa lililokuwa pale sebuleni na mkoba wake akauweka juu ya meza. Akabaki akitafakari juu ya kumkuta Getruda na mchumba wake John Bosho wakiwa wamekaa pamoja.



    Hata hivyo baada ya kukaa kwa muda, Anita alinyanyuka na kuingia chumbani kwake ili kubadili nguo na kuendelea na ratiba nyingine ya usiku ule.  Alipomaliza kubadili na kuvalia upande wa kitenge, akaingia bafuni na kuoga. Alipomaliza kuoga akarudi tena sebuleni ambako alifungua friji na kuchukua soda moja aina ya Mirinda na kukaa tena kwenye sofa.



    Anita aliendelea kunywa soda taratibu, kwani hakuwa na hamu ya kula chakula kabisa, au tusema aliamua kutokula chochote kwa siku ile. Alichokuwa anawaza ni kuachana na mchumba wake, John Bosho mara moja, na pia kuvunja urafiki wake na rafiki yake, Getruda, ambaye kwa muda ule alimfananisha na msaliti aliyeingilia penzi lake.



    Ili aweze kuyapunguza mawazo yale, Anita aliwasha runinga na kuendelea kuangalia vipindi vilivyokuwa vinaendelea ingawa ni kwamba alikuwa haelewi chochote zaidi ya kuona kama ni kivuli tu kilichokuwa mbele yake. Mawazo yalikuwa yamemzidi kupita kiasi, hata hivyo, hakupenda mawazo hayo yamwandame zaidi, isipokuwa alichukua simu yake na kuamua kumpigia simu rafiki yake, Getruda, ili amweleze ukweli juu ya kile kitendo alichokuwa amemfanyia!



            ********



    UPANDE wa pili. Getruda alibaki hana raha kabisa baada ya kukutwa na rafiki yake, Anita, akiwa na mchumba wake, John Bosho. Ukweli ni kwamba aliweza kuiona hatari iliyokuwa inamkabili, akiwaza kuwa ni lazima Anita angemfanyia kitu kibaya ingawa alikuwa ni rafiki yake wa damu, kutokana na kitendo kile alichofanya.



    Getruda alishindwa kabisa hata kumpigia simu rafiki yake, Anita, angalau hata amwombe radhi kwa kile kilichotokea baada ya kumkuta amekaa na mchumba wake, John Bosho. Je, hata angempigia simu, angemwambia nini wakati alikuwa ameshakasirika?”



    Wakati Getruda akiwa katika mawazo yale, simu yake ya mkononi iliita. Akaichukua na kuangalia namba za mpigaji, ambayo ilionyesha ni za shoga yake, Anita! Kwanza kabisa kabla hajaipokea simu ile, mapigo ya moyo wake yakaongezeka huku bado akiiangalia ile simu ilivyokuwa inaita.



    “Haloo…Anita…” Getruda akaipokea.



    “Natumaini hujambo Getruda…” upande wa pili wa simu ukasema.



    “Mimi sijambo…”



    “Umefurahi sana kunichukulia mchumba wangu sivyo?”



    “Hapana Anita…usiseme hivyo!”



    “Unabisha?”



    “Sibishi…isipokuwa…”



    “Sikiliza…” Anita akamwambia na kuendelea. “Sina muda wa kulumbana na wewe! Ukweli ni kwamba umenikwaza sana, na kuanzia leo hii, mimi na wewe urafiki basi, kila mtu aendelee kivyake. Na pia huyo John nakuachia uendelee naye! Nawapa Uhuru!”



    “Usifanye hivyo Anita, hayo ni mambo ambayo yanaweza kuzungumzwa. Tambua kuwa tumetoka mbali sana!”



    “Kama ulikuwa unatambua kuwa tumetoka mbali, usingenifanyia hayo. Hivyo mimi sina mjadala na kwa heri!” Anita akamaliza kusema!



    Akakata simu!

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Mungu wangu!” upande wa pili Getruda akasema na kubaki ameshika simu yake mkononi!



    Getruda alikuwa ameshaupata ujumbe ule kutoka kwa rafik yake, Anita. Hivyo hakuwa na jinsi zaidi ya kukubaliana na uamuzi ule, ingawa kwa masikitiko makubwa!



            ********







    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog